Jumanne, 9 Aprili 2024

Hata saa tisa!

Mathayo 27:45-50 “Basi tangu saa sita palikuwa na giza juu ya nchi yote hata saa tisa. Na kama saa tisa, Yesu akapaza sauti yake kwa nguvu akisema, Eloi, Eloi, lama sabakthani? Yaani, Mungu wangu, Mungu wangu, mbona umeniacha?  Na baadhi yao waliohudhuria, waliposikia, walisema, Huyu anamwita Eliya. Mara mmoja wao akaenda mbio, akatwaa sifongo, akaijaza siki, akaitia juu ya mwanzi, akamnywesha. Wale wengine wakasema, Acha; na tuone kama Eliya anakuja kumwokoa. Naye Yesu akiisha kupaza sauti tena kwa nguvu, akaitoa roho yake.”



Utangulizi:

Moja ya matukio muhimu tunayoweza kuyazingatia katika msimu wa kukumbuka Mateso ya Bwana wetu Yesu Kristo, Kifo chake na kufufuka kwake ni Pamoja na Saa ile aliyokata roho, yaani saa tisa, Karibu kila mwandishi wa Injili anaonyesha tukio hili la kipekee la Yesu kukata roho saa tisa, licha ya kuwepo kwa giza kubwa na la kipekee kuanzia saa sita mpaka saa tisa na kisha saa tisa Ndipo Yesu alikata roho. Tunaweza kuona, tukio hilo likirudiwa tena na tena katika injili nyingine:-

Marko 15:33-34 “Na ilipokuwa saa sita, palikuwa na giza juu ya nchi yote, hata saa tisa. Na saa tisa Yesu akapaza sauti yake kwa nguvu, Eloi, Eloi, lama sabakthani? Maana yake, Mungu wangu, Mungu wangu, mbona umeniacha?”

Luka 23:44-46. “Hapo ilikuwa yapata saa sita, kukawa giza juu ya nchi yote hata saa kenda, jua limepungua nuru yake; pazia la hekalu likapasuka katikati. Yesu akalia kwa sauti kuu, akasema, Ee Baba, mikononi mwako naiweka roho yangu

Tukio la Yesu Kristo kufa saa tisa jioni lina umuhimu mkubwa sana kwa mujibu wa injili na ndio maana limeelezwa na injili zote tatu, tunaelezwa kuwa katika muda huo tofauti na kawaida kulikuwa na giza tangu saa sita hata saa tisa, na saa tisa Yesu alipaza Sauti ya kilio Mungu wangu Mungu wangu Mbona umeniacha, na kisha Yesu alifikia hatua ya kutimiza kusudi lote la ukombozi wa mwanadamu kwa kujitoa dhabihu yeye mwenyewe, kwa ukombozi wa Mwanadamu. Lakini labda swali muhimu linaweza kubakia pale pale kwa nini saa tisa? hilo linatupa nafasi ya kutafakari somo hili hata saa tisa kwa kuzingatia vipengele muhimu vitatu yafuatayo:-


·         Saa tisa katika masimulizi ya kale ya tamaduni za kiyahudi

·         Saa tisa kwa mujibu wa maandiko

·         Hata saa tisa!

 

Saa tisa katika masimulizi ya kale ya tamaduni za kiyahudi

Kwa mujibu wa masimulizi ya Kale Wayahudi waliamini kuwa Mungu alikuwa na tabia ya kumtembelea Adamu katika Bustani ya Edeni, Saa ya jua kupunga, Kwa kiingereza “In the cool of the day” Ruach/yom

Mwanzo 3:8-9 “Kisha wakasikia sauti ya BWANA Mungu, akitembea bustanini wakati wa jua kupunga; Adamu na mkewe wakajificha kati ya miti ya bustani, BWANA Mungu asiwaone. BWANA Mungu akamwita Adamu, akamwambia, Uko wapi?  

Kwa mujibu wa masimulizi ya kiyahudi Muda au wakati wa jua kupunga katika unaitwa YOM ambalo kwa tafasiri wakati wa  jioni ambapo wayahudi walikuwa wanaamini ni mida ya saa tisa, Kwa mujibu wa masimulizi ya kiyahudi Muda huu kwa kawaida Mbingu huwa zinafunguka, na Mungu huwa ana kuwa na shauku ya kuimarisha uhusiano wake na wanadamu, hili ni moja ya jambo la kwanza na muhimu ambalo tunalipata katika Masimulizi ya kiyahudi na ndio maana moja ya saa za maombi katika jumuiya ya kiyahudi ni pamoja na kuomba saa tisa. Meno mawili ya kiebrania yanatumika kuelezea Saa ya jua kupunga in the cool of the day ambalo ni Ruach na Yom yakiwa na maana wakati wa utembeleo wa Roho wa Mungu.

Aidha kweli nyingine ya Masimulizi ya kale ya kiyahudi inasema ni katika muda huu, Mungu alimpa Adamu usingizi Mzito na kuchukua sehemu ya ubavu wake na kumuumba Mwanamke.

Mwanzo 2:21-23 “BWANA Mungu akamletea Adamu usingizi mzito, naye akalala; kisha akatwaa ubavu wake mmoja, akafunika nyama mahali pake, na ule ubavu alioutwaa katika Adamu BWANA Mungu akaufanya mwanamke, akamleta kwa Adamu. Adamu akasema, Sasa huyu ni mfupa katika mifupa yangu, na nyama katika nyama yangu, basi ataitwa mwanamke, kwa maana ametwaliwa katika mwanamume.”

 Usingizi mzito katika lugha ya kiibrania wanatumia neno TARDEMA ambalo maana yake ni hali inayosababishwa na Mungu mwenyewe kwaajili ya kumletea mwanadamu ufunuo muhimu, au kufanya jambo la Muhimu kwa mwanadamu    
          

Masimulizi mengine ni kuwa saa tisa ni muda ambao wayahudi walikuwa wanautumia kwa maombi, kuna vipindi vikubwa vitatu vya maombi katika tamaduni za kiyahudi. Hata manabii na waandishi wa zaburi wana nukuu kadhaa katika maandiko, zinazoashiria kuwa wayahudi walikuwa na vipindi vitatu vya maombi na ambavyo wameendelea kuwa navyo hata siku za leo angalia

Zaburi 55:16-17 “Nami nitamwita Mungu, Na Bwana ataniokoa; Jioni, asubuhi, na adhuhuri nitalalama na kuugua, Naye ataisikia sauti yangu.”

Daniel 6:10-11 “Hata Danieli, alipojua ya kuwa yale maandiko yamekwisha kutiwa sahihi, akaingia nyumbani mwake, (na madirisha katika chumba chake yalikuwa yamefunguliwa kukabili Yerusalemu;) akapiga magoti mara tatu kila siku, akasali, akashukuru mbele za Mungu wake, kama alivyokuwa akifanya tokea hapo.Basi watu hao wakakusanyika pamoja, wakamwona Danieli akiomba dua, na kusihi mbele za Mungu wake   
  

Vipindi hivyo vitatu vya ibada za maombi, ambavyo Wayahudi wanaendelea navyo mpaka leo kwa lugha ya asili ya Kiibrania vinaitwa SHACHARIT, MINCHA NA MAARIV ambavyo tunavichambua kama ifuatavyo:-

1.       Shacharit: - huu ni muda wa maombi ya alfajiri ambapo Wayahudi husali baada ya kupambazuka kwa jua, Maombi haya hufikiriwa kuwa ni maombi ya muhimu sana ambayo wayahudi huamini kuwa wanapokea Baraka kubwa sana, maombi au sala ya alfajiri huambatana na Kusifu, kusoma maandiko hususani Torati. Na hii inasadikiwa kufanyika kati ya muda wa asubuhi mpaka saa tatu na hasa kilele chake ni saa tatu.

 

2.       Mincha: - huu ni Muda wa maombi ya jioni (afternoon) Maombi haya ndiyo ambayo hufanywa saa tisa, ni maombi mafupi sana, ukilinganisha na Maombi ya alfajiri yaani Sacharit, maombi haya ya saa tisa hujumuisha kuomba, kusoma zaburi na kunyamaza kimyaa (Amidah) kusimama kimyaa, nah ii inasadikiwa kufanyika kati ya saa sita mpaka saa tisa na kilele chake hasa kilikuwa saa tisa

 

3.       Maariv au Arvit: Maariv pia huitwa Maarib au Magharibi kwa Kiswahili, Maombi haya yanafanyika baada ya jua kuzama ni kwaajili ya kuukaribisha usiku na kuuaga mchana, maombi haya hujumuisha Baraka, na ukiri wa SHEMA ukiri wa shema ni ukiri unaopatikana katika Kumbukumbu la torati 6:4-5 nimenukuu hapa:-

 

Kumbukumbu 6:4-5 “Sikiza, Ee Israeli; Bwana, Mungu wetu, Bwana ndiye mmoja. Nawe mpende Bwana, Mungu wako, kwa moyo wako wote, na kwa roho yako yote, na kwa nguvu zako zote.”

 

Shema ndio kiini kikuu cha Imani ya kiyahudi, Maombi haya ya Maariv au magharibi kilele chake ni jioni saa kumi na mbili wakati wa kuzama kwa jua.

Kwa hiyo kwa mujibu wa tamaduni za kiyahudi, na dini ya kiyahudi, yanashikiliwa na wayahudi katika maisha yao yote na siku zote, Kwa hiyo kuna saa tatu, kuna saa tisa na kuna saa kumi na mbili, Kwa hiyo  Saa tisa ni moja ya saa nyeti katika tamaduni na dini ya kiyahudi. Wayahudi wengi waliamini kuwa muda huu ni muda mwema sana Saa tisa Muda wa dhabihu ya jioni Mungu husikia kwa haraka sana na hujibu kwa haraka sana, na ni saa ya miujiza mikubwa.

Zaburi 141:1-2 “Ee Bwana, nimekuita, unijie hima, Uisikie sauti yangu nikuitapo. Sala yangu ipae mbele zako kama uvumba, Kuinuliwa mikono yangu kama dhabihu ya jioni.”                        

Saa tisa kwa mujibu wa maandiko:

Nadhani sasa unaweza kupata picha ya umuhimu was aa tisa, ya kwamba ni saa yenye neema ya ajabu, ni saa yenye faida kubwa sana, kila mtu aliyeokolewa ana neema kubwa na amepewa neema ya kuzijua siri za ufalme wa Mungu, lakini kufunuliwa kwa nguvu za ufalme wa Mungu kunategemeana sana na ujuzi wa kanuni, kama vile ambavyo ziko hesabu huwezi kuzifanya bila kujua kanuni, au huwezi kupata majibu bila kujua kanuni, ufunuo kuhusu kanuni unatofautiana kati ya Mtu na mtu, Kadiri unavyozijua kanuni hizo ndio unajiweka katika nafasi kubwa sana ya mafanikio na siri za ufalme wa Mungu na kufaidika kiroho, kwa hiyo maombi ya saa tisa ni ufunuo wa Muhimu sana kwako leo, lakini ili uweze kuwa na ufahamu sasa tufuatane nani katika maandiko kuweza kuona saa hii kwa mujibu wa maandiko:-

-          Ulikuwa ni Muda ambao Bwana alimtembelea Ibrahimu na kuwa na ushirika naye pamoja na Sarah Na kumuahidi kupata mtoto Mwanzo 18:1-2 “BWANA akamtokea Ibrahimu karibu na mialoni ya Mamre, alipokuwa ameketi mlangoni pa hema yake mchana wakati wa hari. Akainua macho yake akaona, na tazama, watu watatu wamesimama mbele yake. Naye alipowaona alipiga mbio kuwalaki kutoka mlangoni pa hema, akainama mpaka nchi, akasema, BWANA wangu, kama nimeona fadhili machoni pako nakuomba usinipite sasa mimi mtumwa wako.” Neno Mchana wakati wa Hari katika kiibrania linatumika tena neno YOM ambalo lina maana ya jioni mida ya saa tisa

 

-          Ulikuwa ni Muda ambao makuhani waliagizwa kutoa dhabihu ya jioni Kutoka 29:38-42 “Basi sadaka utakazozitoa juu ya madhabahu ni hizi; wana-kondoo wa mwaka mmoja wawili siku baada ya siku daima. Mwana-kondoo mmoja utamchinja asubuhi; na mwana-kondoo wa pili utamchinja jioni; tena, pamoja na mwana-kondoo mmoja utatoa vibaba vitatu vya unga mzuri uliochanganyika na mafuta yenye kupondwa, kiasi cha kibaba na robo kibaba; na divai kiasi cha kibaba na robo kibaba, iwe sadaka ya kinywaji. Na huyo mwana-kondoo wa pili utamchinja wakati wa jioni, nawe utamfanyia vivyo kama ile sadaka ya unga ya asubuhi, na kama ile sadaka yake ya kinywaji, iwe harufu nzuri, ni dhabihu ya kusongezwa kwa BWANA kwa njia ya moto. Itakuwa ni sadaka ya kuteketezwa milele katika vizazi vyenu vyote mlangoni pa ile hema ya kukutania mbele ya BWANA; hapo nitakapokutana nanyi, ili ninene na wewe hapo.”

 

-          Ulikuwa ni Muda wa kuchoma au kufukiza uvumba wakati wa dhabihu ya jioni Kutoka 30:7-8 “Na Haruni atafukiza uvumba wa manukato juu yake; KILA SIKU ASUBUHI atakapozitengeneza zile taa, ataufukiza. Na Haruni atakapoziwasha zile taa WAKATI WA JIONI, ATAUFUKIZA, UWE UVUMBA WA DAIMA mbele za BWANA katika vizazi vyenu vyote.”

 

2Nyakati 13:11 “nao humtolea Bwana kila asubuhi, na kila jioni, sadaka za kuteketezwa na fukizo la manukato; mikate ya wonyesho pia huiweka kwa taratibu yake juu ya meza takatifu, na kinara cha dhahabu chenye taa zake, kuwaka kila jioni; kwa maana sisi twayalinda malinzi ya Bwana, Mungu wetu; bali ninyi mmemwacha.”

 

Luka 1:8-14 “Basi ikawa, alipokuwa akifanya kazi ya ukuhani katika taratibu ya zamu yake mbele za Mungu, kama ilivyokuwa desturi ya ukuhani, kura ilimwangukia kuingia katika hekalu la Bwana ili kufukiza uvumba. Na makutano yote ya watu walikuwa wakisali nje saa ya kufukiza uvumba. Akatokewa na malaika wa Bwana, amesimama upande wa kuume wa madhabahu ya kufukizia. Zakaria alipomwona alifadhaika, hofu ikamwingia. Lakini yule malaika akamwambia, Usiogope, Zakaria, maana dua yako imesikiwa, na mkeo Elisabeti atakuzalia mtoto mwanamume, na jina lake utamwita Yohana.Nawe utakuwa na furaha na shangwe, na watu wengi watakufurahia kuzaliwa kwake.”

 

-          Ulikuwa ni Muda ambao Eliya alimuomba Mungu dhidi ya manabii wa baali katika mlima Karmel na Mungu akamjibu kwa moto kutoka mbinguni 1Wafalme 18:36-39 “Ikawa, wakati wa kutoa dhabihu ya jioni, Eliya nabii akakaribia, akasema, Ee Bwana, Mungu wa Ibrahimu, na wa Isaka, na wa Israeli, na ijulikane leo ya kuwa wewe ndiwe Mungu katika Israeli, na ya kuwa mimi ni mtumishi wako, na ya kuwa nimefanya mambo haya yote kwa neno lako. Unisikie, Ee Bwana, unisikie, ili watu hawa wajue ya kuwa wewe, Bwana, ndiwe Mungu, na ya kuwa wewe umewageuza moyo wakurudie. Ndipo moto wa Bwana ukashuka, ukaiteketeza sadaka ya kuteketezwa, na kuni, na mawe, na mavumbi, ukayaramba yale maji yaliyokuwamo katika mfereji. Na watu wote walipoona, wakaanguka kifudifudi; wakasema, Bwana ndiye Mungu, Bwana ndiye Mungu.”

 

-          Ulikuwa ni Muda huu ambao Ezra aliomba Maombi ya toba na maombezi yaliyoleta uamsho mkubwa sana miongoni mwa jamii ya Wayahudi waliokuwa wamerudi nyuma Ezra 9:4-8 “Ndipo wakanikusanyikia watu wote walioyatetemekea maneno ya Mungu wa Israeli, kwa sababu ya lile kosa la watu wa uhamisho; nami nikaketi kwa mshangao hata wakati wa sadaka ya jioni. Na wakati wa sadaka ya jioni nikainuka baada ya kunyenyekea kwangu, nguo yangu na joho yangu zimeraruliwa, nikaanguka magotini nikakunjua mikono yangu mbele za Bwana, Mungu wangu; nikasema, Ee Mungu wangu, nimetahayari, naona haya kuinua uso wangu mbele zako, Mungu wangu; kwa maana maovu yetu ni mengi, hata yamefika juu ya vichwa vyetu, na hatia yetu imeongezeka na kufika mbinguni. Tangu siku za baba zetu tumekuwa na hatia kupita kiasi hata leo; na kwa sababu ya maovu yetu sisi, na wafalme wetu, na makuhani wetu, tumetiwa katika mikono ya wafalme wa nchi hizi, tumepigwa kwa upanga, tumechukuliwa mateka, tumenyang'anywa mali zetu, tumetiwa haya nyuso zetu, kama hivi leo. Na sasa kwa muda kidogo tumeneemeshwa na Bwana, Mungu wetu, hata akatuachia mabaki yaokoke, akatupa msumari katika mahali pake patakatifu. Mungu wetu atutie nuru machoni mwetu, tuburudike kidogo katika kufungwa kwetu.”

 

-          Ulikuwa ni Muda ambao Daniel nabii aliletewa majibu ya maombi yake kupitia malaika Gabriel Daniel 9:20-22 “Basi hapo nilipokuwa nikisema, na kuomba, na kuiungama dhambi yangu, na dhambi ya watu wangu Israeli, na kuomba dua yangu mbele za Bwana, Mungu wangu, kwa ajili ya mlima mtakatifu wa Mungu wangu; naam, nilipokuwa nikinena katika kuomba, mtu yule, Gabrieli, niliyemwona katika njozi hapo kwanza, akirushwa upesi, alinigusa panapo wakati wa dhabihu ya jioni. Akaniagiza, akaongea nami, akasema, Ee Danieli, nimetokea sasa, ili nikupe akili upate kufahamu.”

 

-          Ulikuwa ni Muda ambao Yesu Kristo alikuwa ameimaliza kazi yote Pazia la hekalu lilipasuka na Yesu akakata roho kwa kuikabidhi roho yake mikononi mwa Baba Luka 23:44-46. “Hapo ilikuwa yapata saa sita, kukawa giza juu ya nchi yote hata saa kenda, jua limepungua nuru yake; pazia la hekalu likapasuka katikati. Yesu akalia kwa sauti kuu, akasema, Ee Baba, mikononi mwako naiweka roho yangu

 

-          Ulikuwa ni Muda ambao Petro na Yohana walikuwa wakihudhuria maombi katika hekalu na Kiwete akaponywa na ukawa ndio muujiza wa kwanza katika kanisa la kwanza ulioambatana na uamsho mkubwa na kuokolewa kwa watu wengi zaidi Matendo 3:1-7 “Basi Petro na Yohana walikuwa wakikwea pamoja kwenda hekaluni, saa ya kusali, saa tisa. Na mtu mmoja aliyekuwa kiwete toka tumboni mwa mamaye alichukuliwa na watu, ambaye walimweka kila siku katika mlango wa hekalu uitwao Mzuri, ili aombe sadaka kwa watu waingiao ndani ya hekalu. Mtu huyu akiwaona Petro na Yohana wakiingia hekaluni aliomba apewe sadaka. Na Petro, akimkazia macho, pamoja na Yohana, akasema, Tutazame sisi. Akawaangalia, akitaraji kupata kitu kwao. Lakini Petro akasema, Mimi sina fedha, wala dhahabu, lakini nilicho nacho ndicho nikupacho. Kwa jina la Yesu Kristo wa Nazareti, simama uende. Akamshika mkono wa kuume, akamwinua, mara nyayo zake na vifundo vya miguu yake vikatiwa nguvu.”

 

-          Ulikuwa ni Muda ambao Kornelio  Mmataifa aliyekuwa anaomba na kutoa sana sadaka alipata utembeleo wa malaika akiagizwa na Mungu, kumuita Petro aje kumueleza habari za Kristo Matendo 10:1-6 “Palikuwa na mtu Kaisaria, jina lake Kornelio, akida wa kikosi kilichoitwa Kiitalia, mtu mtauwa, mchaji wa Mungu, yeye na nyumba yake yote, naye alikuwa akiwapa watu sadaka nyingi, na kumwomba Mungu daima. Akaona katika maono waziwazi, kama saa tisa ya mchana, malaika wa Mungu, akimjia na kumwambia, Kornelio! Akamtazama sana, akaogopa akasema, Kuna nini, Bwana? Akamwambia, Sala zako na sadaka zako zimefika juu na kuwa ukumbusho mbele za Mungu. Sasa basi, peleka watu Yafa, ukamwite Simoni, aitwaye Petro. Yeye ni mgeni wa mtu mmoja, jina lake Simoni, mtengenezaji wa ngozi, ambaye nyumba yake iko pwani, atakuambia yakupasayo kutenda.”

 

Hata saa tisa!

Luka 23:44-46. “Hapo ilikuwa yapata saa sita, kukawa giza juu ya nchi yote hata saa kenda, jua limepungua nuru yake; pazia la hekalu likapasuka katikati. Yesu akalia kwa sauti kuu, akasema, Ee Baba, mikononi mwako naiweka roho yangu

Nadhani sasa unaweza kuona umuhimu wa saa tisa, kimsingi ilikuwa ni Muda wa kutoa dhabihu ya jioni kwa wayahudi, ilikuwa ni saa ya kinabii, ulikuwa ni muda ambao wayahudi walipiga tarumbeta ya wito wa kwenda hekaluni kusali, Na Yesu yeye ndiye Dhabihu Halisi ya jioni, Alitumia Muda huo huo kukamilisha kazi yake ya ukombozi, Kristo alikuwa amekamilisha mpango wa Mungu wa kurudisha ushirika na wanadamu, ulikuwa ni muda ambao Msimamizi wa Mateso askari yule alimpiga Yesu Mkuki wa ubavuni ili kuthibitisha kama amekwisha kufa, ubavu ule ulitoa maji na damu, ambayo kimsingi ina thamani kubwa sana katika upatanisho wa watu kwa Mungu, Yesu alipewa Mkewe kutoka katika ubavu wake, (ni Kanisa) limezaliwa kutoka katoka moyo wa upendo wa Kristo, tunaona miujiza mingi, muda huo, tunaona watu wakijibiwa maombi muda huo, tunaona ni Muda ambao wayahudi hawakuomba sana walitumia muda mfupi tu, kwanini kwa sababu Mungu ni Mungu aliye karibu anapatikana na zaidi sana ulikuwa ni muda ambao wengi walitembelewa na malaika, kama muda wa usingizi kwa Adamu muda huo watu wengi waliofanya kazi kutwa nzima wanaweza kusinzia kidogo, ni Muda wa muujiza, ni muda wa rehema ni muda wa neema ya Mungu.

-          Mafunuo makubwa kuhusu Mungu yalishushwa saa tisa.

-          Utembeleo mkubwa wa malaika ulifanyika saa tisa.

-          Kupasuka kwa Pazia la Hekalu na watu wakaona patakatifu ilifanyika saa tisa.

-          Ulikuwa ni muda ambao wayahudi walitoa dhabihu ya pili ya mwanakondoo kwaajili ya upatanisho wa dhambi zao, na sasa tukio hilo la kinabii linakamilishwa na Bwana wetu Yesu

-          Dhabihu ya ukombozi wa mwanadamu ilikamilika saa tisa

-          Yesu alitundikwa Msalabani muda wa kutoa dhabihu ya asubuhi na alikufa muda wa kutoa dhabihu ya jioni

-          Ulikuwa muda wa Kujibiwa maombi kwa Eliya na Mungu alijibu kwa Moto.

-          Ulikuwa ni Muda wa Kujibiwa maombi Daniel kwa kutumiwa malaika

-          Ulikuwa ni Muda wa kutembelewa Abrahamu na wageni watatu

-          Ulikuwa Muda wa kufukiza uvumba katika madhabahu ya kufukiza uvumba wakati wa dhabihu ya jioni

-          Ulikuwa ni muda ambao malaika wa Bwana alimtokea Zekaria na kupewa ahadi ya kuzaliwa Yohana

-          Ulikuwa ni Muda wa kusali kwa Petro na Yohana na Muujiza mkubwa kwa kiwete wa miaka 40

-          Ulikuwa ni muda wa utembeleo kwa Kornelio kuona maono ya malaika

-          Miujiza mikubwa ya kubadilika kwa maisha ya watu ilitokea muda huo

-          Ulikuwa ni muda unaowakilisha saa ya kukubaliwa kwa maombi, Maandiko yanaonyesha hakuna mtu aliwahi kukataliwa kujibiwa maombi yake katika muda huo, japo Mungu anatusikia kila wakati.

-          Jambo kubwa la msingi na la Muhimu kuliko yote saa tisa ndio saa ya ukombozi wetu, kwani Yesu alikufa saa tisa na pazia la Hekalu lilipasuka kumpa kila mmoja nafasi ya kuweza kumfikia Mungu moja kwa moja kupitia sadaka iliyotolewa Msalabani na mwanaye Mpendwa, Yesu Kristo.

Saa tisa ilifanya kazi katika agano la kale na katika agano jipya, siwezi kukufundisha kuwa ufanye kitu saa tisa au uabudu saa tisa au uombe saa tisa,  lakini nataka kusema hivi, kila mtu anayeamini katika mateso, kufa na kufufuka kwa Bwana wetu Yesu na kuokolewa hapaswi kuwa gizani kuwa anapaswa kufanya nini muda huo na uzuri wake hauchukui muda mrefu, hivyo hata kama uko kazini, fanya kitu kidogo kwaajili ya Uhusiano wako na Mungu, Nyenyekea utaona miujiza mikubwa na utajua kwanini Yesu alikufa muda huo kifo kibaya sana kwaajili yetu, utajua kwanini pazia la hekalu lilipasuka, na patakatifu pakaonekana hii maana yake nini ni muda ambao unaweza kukikaribia kiti cha neema na kujipatia Rehema kutoka kwake aliyekuumba na nataka nikushuhudie ya kuwa utamuheshimu milele kwa sababu Bwana takupa neema ya kukusaidia wakati wa mahitaji yako, Kwa kweli saa tisa ni saa ambayo unaweza kuamuru muujiza wako, saa tisa ni kama saa ambayo Mungu yuko tayari kuamka na kufanya kitu kwaajili ya mwanadamu, ni saa ambayo tunaweza kusema Mzee hufungua ofisi yake ili asikilize watu wake, Hebu itumie saa hiii kwaajili ya kuamuru Baraka zako. neno hili ni kweli ni nani awezaye kulifahamu?

Waebrania 4:14-16 “Basi, iwapo tunaye kuhani mkuu aliyeingia katika mbingu, Yesu, Mwana wa Mungu, na tuyashike sana maungamo yetu. Kwa kuwa hamna kuhani mkuu asiyeweza kuchukuana nasi katika mambo yetu ya udhaifu; bali yeye alijaribiwa sawasawa na sisi katika mambo yote, bila kufanya dhambi. Basi na tukikaribie kiti cha neema kwa ujasiri, ili tupewe rehema, na kupata neema ya kutusaidia wakati wa mahitaji.”

 

Na. Rev. Innocent Samuel Kamote

Mkuu wa wajenzi mwenye Hekima       



Jumapili, 7 Aprili 2024

Mpaka mlima wa Mizeituni!


Luka 22:39-44 “Akatoka akaenda mpaka mlima wa Mizeituni kama ilivyokuwa desturi yake; wanafunzi wake nao wakafuatana naye. Alipofika mahali pale aliwaambia, Ombeni kwamba msiingie majaribuni. Mwenyewe akajitenga nao kama kiasi cha kutupa jiwe, akapiga magoti akaomba, akisema, Ee Baba, ikiwa ni mapenzi yako, uniondolee kikombe hiki; walakini si mapenzi yangu, bali yako yatendeke. Malaika kutoka mbinguni akamtokea akamtia nguvu. Naye kwa vile alivyokuwa katika dhiki, akazidi sana kuomba; hari yake ikawa kama matone ya damu yakidondoka nchini.]



Utangulizi:

Katika msimu huu wa Pasaka bado tunaendelea kujifunza maswala kadhaa muhimu na madogo madogo, ambayo wakati mwingine kwa sababu ya kutazama mfumo mzima wa mateso ya Bwana tunaweza kujikuta ni kama tunayapuuzia, lakini yana umuhimu Mkubwa, leo nataka kuzungumzia kile ambacho kimejitokeza katika Mlima wa Mizeituni sehemu iitwayo Gethsemane na kuhusiana na tukio zima la Yesu Kristo kuwa na huzuni na kuingia katika maombi lakini zaidi sana hari yake kuwa kama matone ya damu.  Mahali hapa muhimu panaitwa Mlima wa Mizeituni, lakini vilevile sehemu muhimu ya mlima huu wa mizeituni pia panajulikana kama Bustani iitwayo Gethsemane.  

Mathayo 26:36-39 “Kisha Yesu akaenda pamoja nao mpaka bustani iitwayo Gethsemane, akawaambia wanafunzi wake, Ketini hapa, hata niende kule nikaombe. Akamchukua Petro na wale wana wawili wa Zebedayo, akaanza kuhuzunika na kusononeka. Ndipo akawaambia, Roho yangu ina huzuni nyingi kiasi cha kufa; kaeni hapa, mkeshe pamoja nami. Akaendelea mbele kidogo, akaanguka kifulifuli, akaomba, akisema, Baba yangu, ikiwezekana, kikombe hiki kiniepuke; walakini si kama nitakavyo mimi, bali kama utakavyo wewe.”

Mahali hapo ndio mahali ambapo kimsingi tunaweza kusema ushindi halisi wa Msalaba ulikoanzia, akiwa hapo kumbuka kuwa msaliti ndio alikuwa amekwenda kuwaleta maadui wa kumkamata Yesu, Hapa ndio mahali ambapo, Pia angekamatwa, hapa ndio mahali ambapo angeweza kukata tamaa, hapa ndio mahali ambapo alihitaji msaada wa Mungu, Malaika na wanadamu, Ndipo mahali ambapo angehitaji maombi kutoka kwa wenzake wa karibu ambao kimsingi walilala, hapa ndipo mahali ambapo wale walioahidi kwenda naye gerezani na hata kuwa tayari kufa naye walimkimbia, Hapa ndio mahali ambapo alizidiwa na msongo wa mawazo, hapa ndipo mahali ambapo shetani alisema naye kuhusu msalaba kama anaweza kuukabili au kukinywea kikombe cha mateso, hapa ndio mahali ambapo mipango ya adui iliyokuwa mibaya ilikuwa inaenda kufanikiwa, Ndipo mahali ambapo alitiwa nguvu na kukubaliana kuukabili Msalaba, Kimsingi ni kama Yesu alikuwa hapa katika chumba cha wangonjwa mahututi, mgonjwa ambaye anapambania uhai wake aishi ama afe na kisha mgonjwa anakubali kifo kwa Amani, kwa hiyo mlima wa mizeituni, Bustani ya Gethsemane ni eneo la maamuzi magumu. Ni eneo ambalo wakati na Muda muafaka wa ukombozi wa mwanadamu unaenda kuanza, ni eneo la mapito ya moyoni. Na ya kihisia, na ya hofu na ya kutisha zaidi kuliko hata msalaba wenyewe. Kila mwanadamu katika maisha yake huwa anapitia katika bustani hii, kwa namna moja ama nyingine, ni mahali ambapo tunapaswa kuruhusu Mapenzi ya Mungu yatimizwe! Tunajifunza somo hili, Mpaka mlima wa Mizeituni kwa kuzingatia vipengele viwili vifuatavyo:-

 

·         Mlima wa Mizeituni, Bustani iitwayo Gethsemane

·         Mpaka mlima wa Mizeituni

 

Mlima wa Mizeituni, Bustani iitwayo Gethsemane

Ni Muhimu kufahamu kuwa Neno la Mungu, limekuja kwetu kwa uweza wa Roho Mtakatifu, na Ni Roho huyu wa Mungu aliyewaongoza waandishi kuweka rekodi hizi kwa kusudi la kutufundisha maswala mbali mbali. Katika injili zote tunaona wakiwa wameelezea kuhusiana na Mahali hapa alipokamatwa Yesu, Pakiwa panajulikana kama mlima wa Mizeituni, au bustani ya Gethsemane lakini pia panaitwa Mahali pale, Kama ilivyo umuhimu wa Golgotha au Kalvari, Mlima wa Mizeituni na hasa hapo Gethsemane pana umuhimu mkubwa sana katika safari ya ukombozi wa mwanadamu.

Mathayo 26:30 “Nao walipokwisha kuimba, wakatoka nje kwenda mlima wa Mizeituni.”

Luka 22:39 “Akatoka akaenda mpaka mlima wa Mizeituni kama ilivyokuwa desturi yake; wanafunzi wake nao wakafuatana naye.”

Marko 14:26 “Nao walipokwisha kuimba walitoka kwenda mlima wa Mizeituni.”

Kwa hiyo tunaona Injili zote zikitaja habari za Mlima wa Mizeituni, Ni mlima maarufu na wa zamani sana una ukubwa wa kama kilomita mbili hivi, mlima huu uko upande wa Mashariki mwa mji wa Yerusalem, Mlima huu una urefu wa mita 78 au futi 250 ni mrefu kuliko mlima wa hekalu, na hivyo ni eneo zuri ambalo unaweza kukaa na kuliangalia hekalu vizuri, Yesu alipenda kuutumia mlima huu kwa maombi, kwa hiyo palikuwa ni mahali ambapo alipendelea kupatembelea mara kwa mara akiwa Yerusalem na alitumia mlima huo kufanya maombi, mlima unaitwa mlima wa mizeituni kwa sababu unafunikwa na miti hiyo ya mizeituni na kulifanya eneo hilo kupendeza kwa ukijani wa Miti hiyo, Mahali hapa Ndipo mahali ambapo Yesu alipatumia kupaa mbinguni angalia

Matendo 1:9-12 “Akiisha kusema hayo, walipokuwa wakitazama, akainuliwa, wingu likampokea kutoka machoni pao. Walipokuwa wakikaza macho mbinguni, yeye alipokuwa akienda zake, tazama, watu wawili wakasimama karibu nao, wenye nguo nyeupe, wakasema, Enyi watu wa Galilaya, mbona mmesimama mkitazama mbinguni? Huyu Yesu aliyechukuliwa kutoka kwenu kwenda juu mbinguni, atakuja jinsi iyo hiyo mlivyomwona akienda zake mbinguni. Kisha wakarudi kwenda Yerusalemu kutoka mlima ulioitwa wa Mizeituni, ulio karibu na Yerusalemu, wapata mwendo wa sabato.”

Na ni katika mlima huu huu Yesu atakaporudi atashukia hapo akitokea mbinguni na kufanya vita na Mpinga Kristo, na kusimamisha utawala wake, kwa hiyo Mlima huu ni mlima wa kihistoria katika ukombozi wa mwanadamu na utawala wa Mungu yaani ufalme wa Mungu.  

Zekaria 14:3-4 “Hapo ndipo atakapotokea Bwana, naye atapigana na mataifa hayo, kama vile alipopigana zamani siku ya vita. Na siku hiyo miguu yake itasimama juu ya mlima wa Mizeituni, unaoelekea Yerusalemu upande wa mashariki, nao mlima wa Mizeituni utapasuka katikati yake, upande wa mashariki na upande wa magharibi; litakuwako huko bonde kubwa sana; na nusu ya mlima ule utaondoka kwenda upande wa kaskazini, na nusu yake itaondoka kwenda upande wa kusini.”

Kwa hiyo mlima wa mizeituni ni mahali, muhimu sana katika unabii na historia nzima ya ukombozi wa mwanadamu na kusimama kwa serikali ya kiungu yaani ufalme wa Mbinguni, kwa msingi huo Yesu hakwenda tu katika mlima wa mizeituni kwa bahati mbaya, katika eneo hili la Mlima wa Mizeituni juu ilikuweko sehemu ambayo ilikuwa na bustani nzuri na sehemu hiyo iliitwa Gethsemane, kwa hiyo utaweza kuona tena waandishi wa Injili wakiitaja sehemu hiyo angalia tena katika neno la Mungu hususani baadi ya vitavu vya injili.

Mathayo 26:36 “Kisha Yesu akaenda pamoja nao mpaka bustani iitwayo Gethsemane, akawaambia wanafunzi wake, Ketini hapa, hata niende kule nikaombe.”

Marko 14:32 “Kisha wakaja mpaka bustani iitwayo Gethsemane; akawaambia wanafunzi wake, Ketini hapa muda niombapo.”      

Kwa hiyo katika mlima huo wa mizeituni vilevile kulikuwako bustani ambayo iliitwa Gethsemane na Luka anapaita mahali pale hii ni kwa sababu mahali hapo palikuwa ni maarufu sana hata leo

Luka 22:40 “Alipofika mahali pale aliwaambia, Ombeni kwamba msiingie majaribuni.”

Kwa Msingi huo ni muhimu kufahamu kuwa eneo hili muhimu katika historia ya ukombozi wa mwanadamu, linaitwa Mlima wa Mizeituni, lakini Pia Bustani ya Gethsemane, lakini Luka anapaita mahali pale, na kuonyesha kuwa Yesu alikuwa na desturi ya kwenda katika eneo hilo mara kadhaa, eneo hili kwa maelezo ya kale na katika injili ya Yohana palikuwa ng’ambo ya kijito Kedroni, ambapo ndipo bustani hii ilipokuwepo na Yesu alipachagua kama mahali pa maombi unaweza kuona

Yohana 18:1 “Alipokwisha kusema hayo, Yesu alitoka pamoja na wanafunzi wake kwenda ng'ambo ya kijito Kedroni, palipokuwapo bustani; akaingia yeye na wanafunzi wake.”

Eneo hili linaloitwa GETHSEMANE ambalo ni jina lenye asili ya Kiaram ambalo maana yake Sehemu ya kukamulia mafuta, (oil Press) kwa hiyo uko uwezekano ya kuwa katika bustani ile ya Mizeituni, kulikuweko na mashine za kukamulia mafuta ya zeituni,  na ndio sababu pakaitwa pia GETHSEMANE, lakini vile vile kwanini Luka anapaita MAHALI PALE, mahali hapo palikuwa na historia maarufu ya watu hasa Mfalme mkuu Daudi kwenda kuabudu, lakini sio hivyo tu Ni eneo ambalo Daudi aliposalitiwa na Mwanae Absalom alikimbia na kuvuka mto huu yeye na watu wake na wakapanda mlima huu wa mizeituni wakiwa wanalia sana, wakiwa hawana viatu na wakiwa wamejifunika nguo zao vichwani  mahali hapa kimsingi palikuwa na sehemu ambapo Mungu alikuwa akiabudiwa, Lakini Mfalme Daudi na watu wake walipanda mahali hapa wakiwa wamekata tamaa, wakiwa wanalia machozi, wakiwa hawajui mbele yao itakuwaje. Unaweza kuona katika andiko hili:-

2Samuel 15:30-32 “Daudi akapanda akishika njia ya kuupandia mlima wa Mizeituni, akilia alipokuwa akipanda; naye alikuwa amejifunika kichwa chake, akaenda hana viatu; na watu wote waliokuwa pamoja naye wakajifunika vichwa vyao, kila mmoja wao, wakapanda juu, wakilia walipopanda Mtu mmoja akamwambia Daudi ya kwamba, Ahithofeli yu katika hao waliopatana na Absalomu; Daudi akasema, Ee Bwana, nakusihi, uligeuze shauri la Ahithofeli liwe ubatili. Ikawa, Daudi alipofika juu, hapo Mungu alipoabudiwa, tazama, Hushai, Mwarki, akaja kumlaki na joho Lake Limeraruliwa, tena ana udongo kichwani mwake.               

Kwa hiyo unaweza kuona Gethsemane katika mlima wa mizeituni. Zaituni zilikamuliwa na zikatoa mafuta, lakini vilevile ulikuwa ni mlima wa kutoa machozi, Daudi na watu wake walipanda mlima huu huku wanalia, na Yesu alipanda mlima huu akiwa Analia, Daudi alipanda mlima huu akiwa amekata tamaa na kupoteza matumaini akiwa amesalitiwa na Mwanae Absalom na Yesu anapanda mlima huu akiwa amekata tamaa na anapoteza tumaini kuukabili Msalaba akiwa amesalitiwa na mmoja ya Mwanafunzi wake Muhimu, huku roho yake ikiwa ina huzuni mno

Mpaka mlima wa Mizeituni

Luka 22:39-44 “Akatoka akaenda mpaka mlima wa Mizeituni kama ilivyokuwa desturi yake; wanafunzi wake nao wakafuatana naye. Alipofika mahali pale aliwaambia, Ombeni kwamba msiingie majaribuni. Mwenyewe akajitenga nao kama kiasi cha kutupa jiwe, akapiga magoti akaomba, akisema, Ee Baba, ikiwa ni mapenzi yako, uniondolee kikombe hiki; walakini si mapenzi yangu, bali yako yatendeke. Malaika kutoka mbinguni akamtokea akamtia nguvu. Naye kwa vile alivyokuwa katika dhiki, akazidi sana kuomba; hari yake ikawa kama matone ya damu yakidondoka nchini.]

Tunaona katika andiko letu la msingi kuwa Yesu akaenda pamoja na wanafunzi wake mpaka mlima wa mizeituni, Mahali hapa Yesu alikuwa ameelemewa na Huzuni, Huzuni kubwa kwa sababu anakabiliwa na kifo na sio kifo cha kawaida ni kifo cha msalaba, hakuna mauti mbaya kama mauti ya msalaba, katika historia za hukumu ya kifo, kila taifa lilikuwa lina namna yake ya kuua

Waingereza mtu alipohukumiwa kifo walitumia kitanzi, wakati warumi walitumia shoka lililotundikwa, na wayahudi walitumia kupiga mawe mpaka kifo, warumi walikuwa na hukumu nyingine ya kifo kwa raia asiyekuwa Mrumi ambayo ilikuwa ni kumtundika msalabani, kifo hiki kilikuwa ni kibaya zaidi kwa sababu ni mauti ya polepole, ilikuwa pia ni mauti ya aibu, kwa sababu watu walisulubiwa wakiwa tupu na kudhalilishwa, wayahudi waliamini kuwa Mungu hawezi kuruhusu mtu mwema kufa msalabani, mtu aliyehukumiwa kifo cha msalabani alihesabika kuwa amelaaniwa,

Wagalatia 3:13-14 “Kristo alitukomboa katika laana ya torati, kwa kuwa alifanywa laana kwa ajili yetu; maana imeandikwa, Amelaaniwa kila mtu aangikwaye juu ya mti; ili kwamba baraka ya Ibrahimu iwafikilie Mataifa katika Yesu Kristo, tupate kupokea ahadi ya Roho kwa njia ya imani.”

Kwa hiyo katika mawazo ya Kristo kama Mwana wa Mariam yaani kibinadamu mauti hii ilikuwa ni ya kuiepuka, angetamani sana kikombe hiki kimuepuka aliomba kwa hisia kali sana na hapa alikuwa amejawa na msongo wa mawazo, na ni katika eneo hilo hilo ambapo zaituni zilikuwa zinakamuliwa Yesu alikamuliwa na msongo wa mawazo, kiasi cha kutoka jasho (Hari) la damu, tukio hili kisayansi linaitwa Agony – ambalo maana yake ni Msongo mkubwa wa mawazo unaoathiri hali halisi ya mwili kiasi cha mishipa ya damu kuzidiwa na kupanuka kwa vinyeleo na kuruhusu jasho na damu kutoka, tukio hili liliweza kuelezewa na Luka pekee kwa vile yeye alikuwa tabibu, Kwa hiyo Yesu alikuwa ameleemewa na huzuni kubwa kwa sababu aina ya mateso ilikuwa mbaya kubebeka, na malaika walikuja kumtia nguvu kuwa anapaswa kubeba, kwa hiyo tunapata picha hii Yesu alipokuwa Gethsemane

-          Ni mahali ambapo mtu anaelemewa na huzuni kubwa na msongo mkubwa wa mawazo

-          Ni mahali ambapo mtu anakuwa amesalitiwa na kuachwa peke yake

-          Ni mahali ambapo unajaribu kuomba msaada watu hata wakuombee na wanalala

-          Ni mahali ambapo mtu unakata tamaa na kupoteza matumaini

-          Ni mahali ambapo unaweza kuchanganyikiwa kwa sababu mipango ya adui ndiyo inayokwenda kufanikiwa

-          Ni mahali ambapo ni kama Mungu anasikia maombi ya adui zako na mipango yao na ya kwako haisikiwi

-          Ni mahali ambapo hakuna faraja kutoka upande wowote

-          Ni mahali ambapo shetani angependa ubaki hapo ili akulize akukamue

-          Ni mahali ambapo manabii walipanda wakiwa wanalia, machozi wamekata tamaa

-          Ni mahali ambapo Imani yako inakamuliwa ili ikiwezekana iishe na urudie hapo

-          Ni mahali ambapo pamejaa mashaka na marafiki wamekuacha peke yako

-          Ni mahali ambapo ni kama uko chumba cha wagonjwa mahututi na unaota ndoto za kugombea uhai au kifo

-          Ni mahali ambapo huwezi kuamua mambo, na mambo yako yanaamuliwa na adui zako

-          Ni mahali ambapo unachokiona mbele yako ni kifo tu maombi hayajibiwi

-          Ni mahali ambapo ni kama maamuzi yamepita na huwezi hata kukata rufaa tena

-          Ni mahali ambapo utatiwa mikononi mwa adui na rafiki zako wote watakukimbia

-          Ni mahali ambapo unakutana na vita ya kiakili, kihisia na kiroho, na ni mahali pa maamuzi magumu!

Mungu katika hekima yake huruhusu nyakati Fulani na sisi katika maisha yetu tupite tupande mpaka mlima wa Mizeituni, tuende mpaka Gethsemane tukakamuliwe huko, tukalizwe huko, akili zetu zizungumze na shetani, huku Mungu akiwa kimyaa, Katika hali ya kawaida wakati wa mapito na mateso huwa hauonekani kuwa ni wakati mzuri, unakuwa ni wakati wa kukamuliwa, unakuwa ni wakati wa taarifa mbaya, unakuwa ni wakati wa kuamua kufanya mapenzi ya Mungu au kuyaacha taarifa njema ni kuwa Yesu hakukata tamaa, Yesu hakuvunjika moyo na malaika wa Bwana walikuja kumtia nguvu na akawa yuko tayari kuyakabili mateso ya Msalaba, Daudi alilia katika mlima huu, lakini alifanikiwa kujipanga na kukabiliana na Absalom na Mungu alimpa ushindi, Mungu alijibu maombi ya Yesu kwa kumtia nguvu aukabili Msalaba lakini alijua ya kuwa siku ya tatu atamfufua na kumpeleka katika maisha yasiyozuilika  Ushindi wa maisha yetu na furaha ya kweli hupatikana, pia kwa kupitia njia ya mateso,  tumepewa sio kumwamini tu bali na kuteswa kwaajili yake

Wafilipi 1:28-29 “wala hamwaogopi adui zenu, katika neno lo lote; kwao hao ni ishara mathubuti ya kupotea, bali kwenu ninyi ni ishara ya wokovu, huo utokao kwa Mungu. Maana mmepewa kwa ajili ya Kristo, si kumwamini tu, ila na kuteswa kwa ajili yake;”                

Mungu atatuacha tupite katika wakati Mgumu, ambao utatuletea ushindi mkubwa sana na hivyo hatupaswi kuogopa tunapopita Gethsemane wakati ambapo umeachwa peke yako na hakuna wa kukushika mkono usiogope Yesu Kristo anaijua njia hiyo na ni yeye aliyesema Twendeni mpaka mlima wa mizeituni mlima huu sio wa mateso pekee bali ni mlima wa ushindi, ni mlima wa mahali ambapo sio Yesu atakamatwa tu, na kugongwa kisigino, lakini ni mahali ambapo Yesu atakanyaga tena na mlima huu utapasuka na watachinjiliwa mbali adui zake ni mlima ambapo ufalme wa Mungu utastawi, kumbuka muda wa kupita hapa sio mrefu ni mfupi sana

1Petro 5:8-11 “Mwe na kiasi na kukesha; kwa kuwa mshitaki wenu Ibilisi, kama simba angurumaye, huzunguka-zunguka, akitafuta mtu ammeze. Nanyi mpingeni huyo, mkiwa thabiti katika imani, mkijua ya kuwa mateso yale yale yanatimizwa kwa ndugu zenu walioko duniani. Na Mungu wa neema yote, aliyewaita kuingia katika utukufu wake wa milele katika Kristo, mkiisha kuteswa kwa muda kidogo, yeye mwenyewe atawatengeneza, na kuwathibitisha, na kuwatia nguvu. Uweza una yeye hata milele na milele. Amina.”

Baada ya mateso ya kihisia pale Gethsemane Yesu alitiwa nguvu kuukabili Msalaba, alikwenda msalabani na alipitia dhihaka na mateso akiwa ana utulivu mkubwa sana akijua faida ya mateso yale na kufufuka kwake

-          Alikuwa na nguvu ya kuwaombea maadui zake

-          Alikuwa na nguvu ya kuruhusu majambazi waende peponi

-          Alikuwa na nguvu ya kutangaza kuwa kazi ya ukombozi umekamilika

-          Alikuwa na nguvu ya kukabidhi roho yake kwa Amani akijua ya kuwa Baba yake atamfufua

-          Alikuwa na nguvu ya kuruhusu pazia la hekalu kupasuka na watu kuifikia neema ya Mungu

-          Alikuwa na nguvu ya kufufua watu waliokufa zamani na miili yao kuonekana kwa muda

-          Alikuwa na nguvu dhidi ya Mauti akitupa waamini wote tumaini kubwa lenye Baraka

-          Alikuwa na nguvu ya kusamehe dhambi

-          Alikuwa na nguvu ya kututhibitishia na kutuhakikishia wokovu

-          Alikuwa na nguvu ya kubadilisha maisha ya watu na kuleta mabadiliko makubwa katika jamii zote duniani

-          Alikuwa na nguvu ya kutioa faraja na tumaini kiasi cha kumuwezesha kila mtu kuwa tayari kufa kama yeye

-          Alikuwa na nguvu na mamlaka yote mbinguni na duniani

-          Alikuwa anamejithibitishia kuwa atarudi tena na kukanyaga mlima wa mizeituni

-          Alikuwa na nguvu ya kuwafanya adui zake na wote waliokuwa wakimtesa walikiri hakika alikuwa mwema

Ushindi wote huo hapo juu ni kwa sababu Pale Gethsemane Yesu alikubali Mapenzi ya Mungu, kwamba hata tunapopitia katika njia zilizo ngumu sana hatuachi kuomba tunaomba na baba akiwa kimya tunakubali mapenzi yake yatimizwe

Luka 22:41-43. “Mwenyewe akajitenga nao kama kiasi cha kutupa jiwe, akapiga magoti akaomba, akisema, Ee Baba, ikiwa ni mapenzi yako, uniondolee kikombe hiki; walakini si mapenzi yangu, bali yako yatendeke. Malaika kutoka mbinguni akamtokea akamtia nguvu.”  

Ni pale Gethsemane ndipo Yesu alipotengeneza nguvu ya kukabiliana na hali zote zilizokuwa mbele yake kumbuka alisema ombeni kusudi msiingie majaribuni, aliweza kuyashinda majaribu yote na malaika wa Bwana walikuja kumtia nguvu

Ni pale Gethsemane ndipo Yesu alipoonja hisia na mateso yetu ya kibinadamu tunapokuwa taabuni alionyesha uanadamu wake na sisi tunapopita katika majaribu makali anaujua uanadamu wetu, Ni hapa ndipo wanafunzi wa Yesu walipofahamu umuhimu wa maombi, ni hapa ndipo alipowafundisha namna wanavyoweza kukabiliana na ushindi wanapokuwa matatani.

Mathayo 26:41 “Kesheni, mwombe, msije mkaingia majaribuni; roho i radhi, lakini mwili ni dhaifu.”

Ni pale Gethsemane ndipo Yesu alionyesha kuwa kweli yeye ni Mpakwa mafuta kwa sababu alikubali kuukabili msalaba bila vurumai yoyote aliukabili msalaba kwa upole na unyenyekevu mkubwa

Isaya 53:3-7 “Alidharauliwa na kukataliwa na watu; Mtu wa huzuni nyingi, ajuaye sikitiko; Na kama mtu ambaye watu humficha nyuso zao, Alidharauliwa wala hatukumhesabu kuwa kitu. Hakika ameyachukua masikitiko yetu, Amejitwika huzuni zetu; Lakini tulimdhania ya kuwa amepigwa, Amepigwa na Mungu, na kuteswa. Bali alijeruhiwa kwa makosa yetu, Alichubuliwa kwa maovu yetu; Adhabu ya amani yetu ilikuwa juu yake, Na kwa kupigwa kwake sisi tumepona. Sisi sote kama kondoo tumepotea; Kila mmoja wetu amegeukia njia yake mwenyewe; Na Bwana ameweka juu yake Maovu yetu sisi sote. Alionewa, lakini alinyenyekea, Wala hakufunua kinywa chake; Kama mwana-kondoo apelekwaye machinjoni, Na kama vile kondoo anyamazavyo Mbele yao wakatao manyoya yake; Naam, hakufunua kinywa chake.”

Ni pale Gethsemane Ndipo Yesu alipoanza harakati za ukombozi wa mwanadamu kwa kukabiliana na matukio yote kuanzia mahakamani, kusulubiwa kufa na kufufuka akiwa sadaka kamili ya upatanisho na msamaha wa dhambi zetu akitupatanisha sisi na Mungu

1Timotheo 2:5-6 “Kwa sababu Mungu ni mmoja, na mpatanishi kati ya Mungu na wanadamu ni mmoja, Mwanadamu Kristo Yesu; ambaye alijitoa mwenyewe kuwa ukombozi kwa ajili ya wote, utakaoshuhudiwa kwa majira yake.”

Ni Gethsemane ndipo Yesu alipoandaa ukamilisho wa eneo muhimu la huduma yake duniani akionyesha kumtii Mungu hata mauti ya msalaba, akiwa tayari kukamilisha mapenzi ya Mungu, huruma zake kubwa kwa wanadamu na wajibu wake mkubwa kama mwokozi wa ulimwengu jambo ambalo limemletea sifa kubwa sana Mbinguni

Wafilipi 2:5-11 “Iweni na nia iyo hiyo ndani yenu ambayo ilikuwamo pia ndani ya Kristo Yesu; ambaye yeye mwanzo alikuwa yuna namna ya Mungu, naye hakuona kule kuwa sawa na Mungu kuwa ni kitu cha kushikamana nacho; bali alijifanya kuwa hana utukufu, akatwaa namna ya mtumwa, akawa ana mfano wa wanadamu; tena, alipoonekana ana umbo kama mwanadamu, alijinyenyekeza akawa mtii hata mauti, naam, mauti ya msalaba. Kwa hiyo tena Mungu alimwadhimisha mno, akamkirimia Jina lile lipitalo kila jina; ili kwa jina la Yesu kila goti lipigwe, la vitu vya mbinguni, na vya duniani, na vya chini ya nchi; na kila ulimi ukiri ya kuwa YESU KRISTO NI BWANA, kwa utukufu wa Mungu Baba.”

Ndugu msomaji wangu, kumbuka wakati wote unapopitia mateso, ni kama uko Gethsemane, ni kama Mwalimu amekuambia upande mlima wa mizeituni, utakuwepo kwa Muda mfupi na ukimtii Mungu katika wakati huo Mungu, atakupeleka katika maisha ya Gethsemane, na kukupeleka katika maisha yasiyoweza kuzuilika, wote sasa tunaweza kuona umuhimu wa mlima wa mizeituni na eneo la Gethsemane, tunajifunza kujitia nguvu katika Bwana, kuwa na ujasiri na utayari wa kukabiliaba na mambo magumu ambayo kwa kawaida Mungu huyafupiza sana lakini hutupa matokeo mazuri sana tunapokuwa tumeyatii mapenzi yake. Mungu akutie nguvu wakati wote unapopanda mlima wa mizeituni na kupita eneo la kukamuliwa, Malaika wa bwana watakutia nguvu utakuwa na moyo wa ujasiri na utashinda na kuwa msaada mkubwa kwa ulimwengu unaokuzunguka Uongezewe neema!

 

Na. Rev. Mkombozi Innocent Samuel bin Jumaa bin Athumani Sekivunga Kamote

Mkuu wa wajenzi mwenye Hekima



Jumapili, 31 Machi 2024

Maisha yasiyozuilika!


Ufunuo 1:17-18 “Nami nilipomwona, nalianguka miguuni pake kama mtu aliyekufa. Akaweka mkono wake wa kuume juu yangu, akisema, Usiogope, Mimi ni wa kwanza na wa mwisho, na aliye hai; nami nalikuwa nimekufa, na tazama, ni hai hata milele na milele. Nami ninazo funguo za mauti, na za kuzimu.”     




Utangulizi:

Leo ni sikukuu ya Pasaka, ambapo wakristo nchini wanaungana na wakristo wote duniani kuadhimisha kuteswa, kufa na kufufuka kwa Bwana wetu Yesu Kristo kulikotokea zaidi ya miaka 2000 iliyopita Huko Yerusalem Nchini Israel, Katika wakati huu wa Pasaka Leo ni Muhimu kujikumbusha kuwa Mungu ametupa maisha yasiyozuilika, Kristo Yesu alipofufuka ametufundisha na kutukumbusha  kuwa kuna maisha yasiyozuilika, Yesu anatufundisha kupitia kufufuka kwake kuwa yako maisha yasiyozuilika,  na kuwa uko uwezekano wa kuishi maisha yasiyozuilika, Haya ni maisha ambayo Mungu alikusudia kila mmoja ayaishi katika ulimwengu huu ambao una vikwazo vingi sana, Lakini kama mtu akiwa na Yesu ataweza kuishi maisha yasiyoweza kuziilika!  Maisha yasiyozuilika ni maisha ya kushinda vikwazo:-

1Yohana 5:11-13 “Na huu ndio ushuhuda, ya kwamba Mungu alitupa uzima wa milele; na uzima huu umo katika Mwanawe. Yeye aliye naye Mwana, anao huo uzima; asiye naye Mwana wa Mungu hana huo uzima. Nimewaandikia ninyi mambo hayo, ili mjue ya kuwa mna uzima wa milele, ninyi mnaoliamini Jina la Mwana wa Mungu.”

Unaweza kujiuliza kuwa Mchungaji anataka kuzungumzia nini? Je maisha yasiyozuilika nini Ni uzima wa milele? Ama ni kitu gani na kwa vipi maisha hayo yana uhusiano na Yesu aliyefufuka?  Tutachukua muda kujifunza kwa ufupi na kwa kina ili tuweze kuelewa maisha hayo yasiyozuilika kwa kuzingatia vipengele viwili tu vifuatavyo:- 

·         Maana ya maisha yasiyozuilika

·         Maisha yasiyozuilika

Maana ya Maisha yasiyozuilika! 

Tunapozungumzia kuhusu Maisha yasiyozuilika, tunazungumzia kuwa na maisha yasiyo na mipaka, au maisha yanayoshinda vikwazo, maisha ya uhuru na na yaliyojaa neema ya Mungu inayotusaidia kufikia ndoto zetu huku tukishinda kila aina ya kikwazo kinachowekwa na shetani au wanadamu,  Maisha yanayoweza kuwa na ushindi, bila kujali nguvu kutoka nje inasema nini, Unapoyasoma maandiko yanaonyesha wazi kuwa Mpango wa Mungu kwa mwanadamu tangu mwanzo ilikuwa ni aina hii ya maisha na Yesu aliyefufuka anatukumbusha kupitia hatua yake ya kufufuka kuwa yako maisha yasiyozuilika!, Mapena na mara kadhaa Yesu alikuwa amesema atafufuka  na alisema kuwa atafufuka siku ya tatu na mpango huu Yesu alitaka ueleweke wazi kwa wanafunzi wake na hata kwa adui zake na ndio maana alirudia tena na tena maneno yake hayo ona:-

-          Mathayo 16:21-23 “Tangu wakati huo Yesu alianza kuwaonya wanafunzi wake ya kwamba imempasa kwenda Yerusalemu, na kupata mateso mengi kwa wazee na wakuu wa makuhani, na waandishi, na kuuawa, na siku ya tatu kufufuka. Petro akamchukua, akaanza kumkemea, akisema, Hasha, Bwana, hayo hayatakupata. Akageuka, akamwambia Petro, Nenda nyuma yangu, Shetani; u kikwazo kwangu; maana huyawazi yaliyo ya Mungu, bali ya wanadamu.”

 

-          Marko 8:31-32a “Akaanza kuwafundisha kwamba imempasa Mwana wa Adamu kupatikana na mateso mengi, na kukataliwa na wazee, na wakuu wa makuhani, na waandishi, na kuuawa, na baada ya siku tatu kufufuka. Naye alikuwa akinena neno hilo waziwazi.”

 

-          Luka 9:21-22 “Akawaonya, akawakataza wasimwambie mtu neno hilo; akisema, Imempasa Mwana wa Adamu kupata mateso mengi, na kukataliwa na wazee na wakuu wa makuhani na waandishi, na kuuawa na siku ya tatu kufufuka.”

 

-          Mathayo 17:22-23 “Nao walipokuwa wakikaa Galilaya, Yesu akawaambia, Mwana wa Adamu anakwenda kutiwa katika mikono ya watu, nao watamwua, na siku ya tatu atafufuka. Wakasikitika sana.”

 

-          Marko 9:30-32 “Wakatoka huko, wakapita katikati ya Galilaya; naye hakutaka mtu kujua. Kwa sababu alikuwa akiwafundisha wanafunzi wake, akawaambia, Mwana wa Adamu yuaenda kutiwa katika mikono ya watu, nao watamwua; hata akiisha kuuawa, baada ya siku tatu atafufuka. Lakini hawakulifahamu neno lile, wakaogopa kumwuliza.       

 

-          Luka 9:43-45 “Wote wakashangaa, wakiuona ukuu wa Mungu. Nao walipokuwa wakiyastaajabia mambo yote aliyoyafanya, aliwaambia wanafunzi wake, Yashikeni maneno haya masikioni mwenu, kwa kuwa Mwana wa Adamu anakwenda kutiwa katika mikono ya watu. Lakini hawakulifahamu neno lile, likafichwa kwao wasilitambue; wakaogopa kumwuliza maana yake neno lile.”

Kwa hiyo huu ulikuwa ni mpango wa Mungu, Na Bwana Yesu aliusema mapema kwamba kifo hakiwezi kumzuia, hakuna kitu kinaweza kuzuia mpango wake wa kufufuka kutoka kwa wafu, huu ndio ulikuwa ujumbe mkuu wa Yesu, Lakini katika namna ya kushangaza shetani pamoja na majeshi yake yote walikuwa na mpango wao wa kuzuia ili yamkini ikiwezekana Yesu asifufuke ona 

Mathayo 27:62-66 “Hata siku ya pili, ndiyo iliyo baada ya Maandalio, wakuu wa makuhani, na Mafarisayo wakamkusanyikia Pilato, wakasema, Bwana, tumekumbuka kwamba yule mjanja alisema, alipokuwa akali hai, Baada ya siku tatu nitafufuka. Basi amuru kwamba kaburi lilindwe salama hata siku ya tatu; wasije wanafunzi wake wakamwiba, na kuwaambia watu, Amefufuka katika wafu; na udanganyifu wa mwisho utapita ule wa kwanza. Pilato akawaambia, Mna askari; nendeni mkalilinde salama kadiri mjuavyo. Wakaenda, wakalilinda kaburi salama, kwa kulitia lile jiwe muhuri, pamoja na wale askari walinzi.”

Unaona njama zilipangwa na viongozi wa kidini wakishirikiana na serikali ya kirumi kuhakikisha kaburi la Yesu linalindwa salama, Kulindwa salama maana yake ni kulinda kwa uhakika, kuhakikisha kuwa hakuna linalobatilika, lindeni kwa kukakisha kuwa haibiwi, lindeni kwa kuhakikisha kuwa hafufuki!  Kwa hiyo wayahudi walitaka kuhakikisha Yesu anabaki kaburini na hatoki tena na hachomoki kabisa kutoka katiia mpango wake huo, walimuwekea ulinzi waliweka mipaka, waliweka kizuizi, walitaka kuakikisha kuwa hakubadiliki neno, Hata hivyo hawakujua kuwa Yesu aliishi maisha yasiyozuilika na hakuna kitu ambacho kingeweza kumzuia asitoke kaburini, hata kifo hakiwezi kumzuia na kumfanya abaki kaburini, Kristo alikuwa na maisha yasiyozuilika, na kifo kisingeliweza kumzuia hakuna cha kumzuia Yesu katika mpango wake.

Maisha yasiyozuilika    

Mathayo 28:1-7 “Hata sabato ilipokwisha, ikipambazuka siku ya kwanza ya juma, Mariamu Magdalene, na Mariamu yule wa pili, walikwenda kulitazama kaburi. Na tazama, palikuwa na tetemeko kubwa la nchi; kwa sababu malaika wa Bwana alishuka kutoka mbinguni, akaja akalivingirisha lile jiwe akalikalia. Na sura yake ilikuwa kama umeme, na mavazi yake meupe kama theluji. Na kwa kumwogopa, wale walinzi wakatetemeka, wakawa kama wafu. Malaika akajibu, akawaambia wale wanawake, Msiogope ninyi; kwa maana najua ya kuwa mnamtafuta Yesu aliyesulibiwa. Hayupo hapa; kwani amefufuka kama alivyosema. Njoni, mpatazame mahali alipolazwa. Nanyi nendeni upesi, mkawaambie wanafunzi wake, Amefufuka katika wafu. Tazama, awatangulia kwenda Galilaya; ndiko mtakakomwona. Haya, nimekwisha waambia.” 

Yesu alisema atafufuka, na wapinzani wake walitaka kuhakikisha kuwa Yesu hafufuki, waliweka walinzi katika kaburi lake, waliweka muhuri kuhakikisha kuwa hakuna neno linalobatilika lakini Yesu/Mungu akisema neno lake hakuna mtu anaweza kusimama kinyume na makusudi na mpango wa Mungu, Yesu alikuwa akituonyesha wazi kuwa tunaweza kuishi maisha yasiyozuilika, kila anaemwamini Yesu na kuiamini kazi aliyoifanya pale msalabani, atakuwa na maisha yasiyozuilika, sio kifo tu lakini kila kitu kinachojaribu kusimama kinyume na kile unachokusudia kukifanya, au biashara zako, au ndoa yako, au mafanikio yako, au kazi yako, au vyovyote vile, unapaswa kukumbuka kuwa Yesu anatuonyesha njia kuwa hakuna anayeweza kukuwekea mipaka katika maisha yako, Kristo aliyefufuka ni mfano mzuri wa maisha yasiozuilika, tangu mwanzo Mungu alikusudia kuwa watu wake wawe mashahidi wa kazi zake na wakati wote kazi zake na mpango wake hakuna anayeweza kuzuia 

Isaya 43:12-13 “Nimetangaza habari, nimeokoa, nimeonyesha, na hapakuwa mungu wa kigeni kati yenu; kwa sababu hiyo ninyi ni mashahidi wangu, asema Bwana, nami ni Mungu. Naam, tangu siku ya leo, mimi ndiye; wala hapana awezaye kuokoa katika mkono wangu; mimi nitatenda kazi, naye ni nani awezaye kuizuia?

Kufufuka kwa Yesu Kristo ndio ulikuwa ushindi mkubwa sana dhidi ya shetani maajenti wake na kazi zake zote, na ilikuwa ndio kilele cha utekelezaji wa kazi ya ukombozi wa Mwanadamu, kwa hiyo shetani alikuwa anataka kuzuia na kuiwekea mipaka kazi iliyofanywa na Bwana, wakati wote unapokaribia katika mafanikio yako, au inapokaribia kuwa Mungu anataka kubadilisa kabisa mpango wa maisha yako na kukuinua, Kuzimu inataharuki na itahakikisha inapambana na kuzuia  mpango wa Mungu katika maisha yako, wakati huo shetani anasahau kuwa Yesu amekupa maisha yasiyozuilika, Kila mtu aliyeokolewa yuko upande wa Mungu yuko na Bwana na Mungu ametupa maisha yasiyizuilika, Kama hakuna kitu cha kututenga na Upendo wa Mungu ni wazi vilevile kuwa hakuna kitu kitaweza kutuzuia katika jambo lolote lile zingatia kuwa Yesu aliyefufuka anaza mamlaka za mauti na kuzimu na zaidi ya yote yeye ndiye huo ufufuo na uzima sasa jaribu kuwaza na kifikiri nini kinaweza kuzuia maisha yako ? angalia maandiko:- 

Warumi 8:31-39 “Basi, tuseme nini juu ya hayo? Mungu akiwapo upande wetu, ni nani aliye juu yetu? Yeye asiyemwachilia Mwana wake mwenyewe, bali alimtoa kwa ajili yetu sisi sote, atakosaje kutukirimia na mambo yote pamoja naye? Ni nani atakayewashitaki wateule wa Mungu? Mungu ndiye mwenye kuwahesabia haki. Ni nani atakayewahukumia adhabu? Kristo Yesu ndiye aliyekufa; naam, na zaidi ya hayo, amefufuka katika wafu, naye yuko mkono wa kuume wa Mungu; tena ndiye anayetuombea. Ni nani atakayetutenga na upendo wa Kristo? Je! Ni dhiki au shida, au adha, au njaa, au uchi, au hatari, au upanga? Kama ilivyoandikwa, ya kwamba, Kwa ajili yako tunauawa mchana kutwa, Tumehesabiwa kuwa kama kondoo wa kuchinjwa. Lakini katika mambo hayo yote tunashinda, na zaidi ya kushinda, kwa yeye aliyetupenda. Kwa maana nimekwisha kujua hakika ya kwamba, wala mauti, wala uzima, wala malaika, wala wenye mamlaka, wala yaliyopo, wala yatakayokuwapo, wala wenye uwezo, wala yaliyo juu, wala yaliyo chini, wala kiumbe kinginecho chote hakitaweza kututenga na upendo wa Mungu ulio katika Kristo Yesu Bwana wetu.”

Unaona maandiko yanaonyesha ukimuamini Yesu unapewa maisha yasiyozuilika na hakuna cha kutuzuia, hakuna wa kutushitaki, maana wako watu watatafuta mambo ya kukushitaki, walimshitaki Yesu mbona! tena kwa ushahidi wa uongo, watatafuta kukudhihaki, watakufanyia kila kitu kibaya ili yamkini ikiwezekana ukate tamaa, wanaweza kutuhukumu, wanaweza kutupangia aina ya adhabu, wanaweza kutupangia aina ya hukumu, wanaweza kukadiria aina ya maisha yetu, wanaweza kujifanya wana hatima ya maisha yetu kwa vyovyote vile  lakini kumbuka kuwa hawajafa kwaajili yetu,  Yesu ndiye aliyekufa na zaidi ya hayo amefufuka katika wafu, na yuko mkono wa kuume anatuombea, maombi ya Yesu kwaajili yako na yangu hayawezi kukataliwa, yuko mkono wa kuume wa baba kwa sababu hiyo kumbe kufufuka kwake kuna umuhimu mkubwa sana kwa sababu kunatupa maisha yasiyozuilika, kila anayepambana na kusudi la Mungu ndani yako anapaswa kuchukua tahadhari kubwa kwa sababu huenda anataka vita na Mungu, na akipigana na Mungu atajikuta yuko kwenye madhara makubwa kwa sababu tumepewa maisha yasiyozuilika, Wayahudi sio tu walitaka kuzia Yesu asifufuke lakini pia walitaka kuizua kazi yake mtu mmoja mwenye hekima akawaonya wayahudi kuwa waache kupambana na kazi za Yesu, kama walimsindwa Yeye waachie kazi yake ona   

Matendo 5:33-39 “Wao waliposikia wakachomwa mioyo yao; wakafanya shauri kuwaua. Lakini mtu mmoja, Farisayo, jina lake Gamalieli, mwalimu wa torati, mwenye kuheshimiwa na watu wote, akasimama katika baraza, akaamuru mitume wawekwe nje kitambo kidogo, akawaambia, Enyi waume wa Israeli, jihadharini jinsi mtakavyowatenda watu hawa. Kwa sababu kabla ya siku hizi aliondoka Theuda, akijidai ya kuwa yeye ni mtu mkuu, watu wapata mia nne wakashikamana naye; naye aliuawa na wote waliomsadiki wakatawanyika wakawa si kitu.Baada ya mtu huyo aliondoka Yuda Mgalilaya, siku zile za kuandikiwa orodha, akawavuta watu kadha wa kadha nyuma yake, naye pia akapotea na wote waliomsadiki wakatawanyika.Basi sasa nawaambia, Jiepusheni na watu hawa, waacheni; kwa kuwa shauri hili au kazi hii ikiwa imetoka kwa binadamu, itavunjwa, lakini ikiwa imetoka kwa Mungu hamwezi kuivunja; msije mkaonekana kuwa mnapigana na Mungu.”    
          

Pasaka hii ni onyo dhidi ya watu wote wanaokusudia na waliokusudia kushindana na mapenzi ya Mungu, kwa kanisa, kwa watumishi wake, na kwa maisha yako kwamba wajihadhari waache kushughulika na watu wenye maisha yasiyozuilika, mtu aliyeokolewa na kumuamini Bwaa Yesu kuwa bwana na mwokozi wa maisha yake hakuna cha kumzuia hata ukimuua, anapita tu kutoka mautini na kuingia uzimani, 

Yohana 5:24 “Amin, amin, nawaambia, Yeye alisikiaye neno langu na kumwamini yeye aliyenipeleka yuna uzima wa milele; wala haingii hukumuni, bali amepita kutoka mautini kuingia uzimani.”

Hakuna raha kama kuishi maisha yasiyozuilika maana kuna faida nyingi sana, na hatuwezi kuzimaliza zote lakini lakini zote hizi tunapewa kwa sababu Mungu alitaka tuwe na maisha yasiyozuilika  

-          Watashindana nawe na hawatakushinda – Yeremia 1:18-19 “Maana, tazama, nimekufanya leo kuwa mji wenye boma, na nguzo ya chuma, na kuta za shaba, juu ya nchi yote; juu ya wafalme wa Yuda, na juu ya wakuu wake, na juu ya makuhani wake, na juu ya watu wa nchi hii. Nao watapigana nawe; lakini hawatakushinda; maana mimi nipo pamoja nawe, asema Bwana, ili nikuokoe.”

 

-          Kila silaha itakayofanyika juu yako haitafanikiwa – Isaya 54:17 “Kila silaha itakayofanyika juu yako haitafanikiwa na kila ulimi utakaoinuka juu yako katika hukumu utauhukumu kuwa mkosa. Huu ndio urithi wa watumishi wa Bwana, na haki yao inayotoka kwangu mimi, asema Bwana.”

 

-          Hakuna uchawi wala uganga utakuweza – Hesabu 23:23 “Mungu amewaleta kutoka Misri, Naye ana nguvu kama nguvu za nyati. Hakika hapana uchawi juu ya Yakobo, Wala hapana uganga juu ya Israeli. Sasa habari za Yakobo na Israeli zitasemwa, Ni mambo gani aliyoyatenda Mungu!

               

-          Adui atakuja kwa njia moja atatawanyika kwa njia saba - Kumbukumbu 28:7 “Bwana atawafanya adui zako wainukao juu yako kupigwa mbele yako; watakutokea kwa njia moja, lakini watakimbia mbele yako kwa njia saba.”                 

Ndugu yangu unapoadhimisha sikukuu ya pasaka leo, Nakuombea kwa Mungu, na ni maombi yangu kuwa kila mmoja wetu aweze kuishi maisha yasiyozuilika, Yesu Kristo aliyefufuka ana mamlaka ya kuzimu na mauti, hivyo kila amuaminiye maana yake hakuna mtu anakuweza, sio mauti sio kuzimu, wala lolote linaweza kuyafanya maisha yako yakawa na kizuizi, Alipomwambia Yohana asiogope anakuambia na wewe na mimi tusiogope

Ufunuo 1:17-18 “Nami nilipomwona, nalianguka miguuni pake kama mtu aliyekufa. Akaweka mkono wake wa kuume juu yangu, akisema, Usiogope, Mimi ni wa kwanza na wa mwisho, na aliye hai; nami nalikuwa nimekufa, na tazama, ni hai hata milele na milele. Nami ninazo funguo za mauti, na za kuzimu.”     

Pasaka hii Mungu akuondolee vikwazo vya kila aina katika maisha yako na vile utakavyokutana navyo Mungu akupe kuvishinda, Mimi nilikutana na vikwazo vingi na vizuizi vyingi sana katika maisha yangu, huduma na utumishi, lakini hakuna hata kimoja kiliweza kuyazuia maisha yasiyozuilika Bwana anaweza hata kuandaa meza Machoni pa watesi wako na kukupaka mafuta mpaka kikombe chako kikafurika, Ubarikiwe na usihi maisha yasiyozuilika, kukiwa na maji tembea juu ya maji, wakitaka kukukamata pita katikati yao wende zako, wakikutupa katika makanwa ya simba hutatafunwa, wakikutupa katika tanuru la moto hutatekeketa, bahari ikiwa kikwazo bwana atafanya njia, kila iana ya dhiki na mateso na majaribu utayapitia lakini, utatoboa, wakikuzika na kulilinda kaburi ili usifufuke tetemeko na malaika wa bwana atawafanya aduinzako wawe kama wafu nawe utatoka. Kwa nini kwa sababu Yesu ametukirimia Maisha yasiyozuilika, na kwa jina lake kila kikwazo kinachisimama mbele yako kitabomolewa na kusawazishwa katika jina la Yesu. Nakutakia msimu mzuri wa sikukuu ya Pasaka Mungu akutunze!

Rev. Innocent Samuel Kamote

Mkuu wa wajenzi mwenye Hekima.