Jumapili, 2 Juni 2024

Mwanadamu siku zake zi kama majani


Zaburi 103:14-16 “Kwa maana Yeye anatujua umbo letu, Na kukumbuka ya kuwa sisi tu mavumbi. Mwanadamu siku zake zi kama majani; Kama ua la kondeni ndivyo asitawivyo. Maana upepo hupita juu yake, kumbe haliko! Na mahali pake hapatalijua tena.”




Utangulizi:

Ni muhimu kujikumbusha tena na tena Japokuwa haipendezi ya kuwa maisha ya mwanadamu duniani yamefupizwa sana, Kimsingi maisha ya mwanadamu ni mafupi mno ukilinganisha na maisha ya milele, ambayo Mungu amekusudia kuwapa wanadamu kama watamuamini Bwana Yesu,

Yohana 3:16 “Kwa maana jinsi hii Mungu aliupenda ulimwengu, hata akamtoa Mwanawe pekee, ili kila mtu amwaminiye asipotee, bali awe na uzima wa milele.”

Kufupishwa kwa maisha ya mwanadamu kumetokana na Mungu mwenyewe kuyapunguza kama adhabu Baada ya kuongezeka kwa maasi yaani dhambi zetu wanadamu hapa ulimwenguni!

Mwanzo 6:1-3 “Ikawa wanadamu walipoanza kuzidi usoni pa nchi na wana wa kike walizaliwa kwao, wana wa Mungu waliwaona hao binti za wanadamu ya kuwa ni wazuri; wakajitwalia wake wo wote waliowachagua. BWANA akasema, Roho yangu haitashindana na mwanadamu milele, kwa kuwa yeye naye ni nyama; basi siku zake zitakuwa miaka mia na ishirini.”

Mwanzoni mwanadamu alikuwana uwezo wa kuishi kwa karne tisa (9) yaani miaka mia tisa na zaidi, na Mwanadamu aliyepata kuishi sana kuliko wanadamu wote aliitwa Methusela ambaye aliishi miaka 969 (mia tisa sitini na tisa)

Mwanzo 5:22-27 Henoko akaenda pamoja na Mungu baada ya kumzaa Methusela miaka mia tatu, akazaa wana, waume na wake. Siku zote za Henoko ni miaka mia tatu na sitini na mitano. Henoko akaenda pamoja na Mungu, naye akatoweka, maana Mungu alimtwaa. Methusela akaishi miaka mia na themanini na saba, akamzaa Lameki. Methusela akaishi baada ya kumzaa Lameki miaka mia saba na themanini na miwili, akazaa wana, waume na wake. Siku zote za Methusela ni miaka mia kenda na sitini na kenda, akafa.”

Hata hivyo maisha ya mwanadamu siku za leo yamekuwa mafupi zaidi kama maua au majani au mvuke, japokuwa kila mwanadamu anatamani kuishi milele, Kwa msingi huo haijalishi mwanadamu ataishi muda mrefu kiasi gani bado maisha hayo ni mafupi kwa nini kwa sababu maandiko yanasema pia yanaenda kwa kasi sana yaani kama kivuli, kwa hiyo maisha haya hayatoshi, bado uko uhitaji wa maisha ya milele, na ndio maana Mungu katika hekima yake alituumba tuishi milele na kwa sababu hiyo kila mwanadamu kwaasili hapendi kifo milele iko katika mioyo yetu.

Muhubiri 3:11-14 “Kila kitu amekifanya kizuri kwa wakati wake; tena ameiweka hiyo milele ndani ya mioyo yao; ila kwa jinsi mwanadamu asivyoweza kuivumbua kazi ya Mungu anayoifanya, tangu mwanzo hata mwisho. Mimi najua ya kwamba hakuna jema kwao kupita kufurahi, na kufanya mema maadamu wanaishi. Tena ni karama ya Mungu kila mtu apate kula na kunywa, na kujiburudisha kwa mema katika kazi yake yote. Najua ya kwamba kila kazi aifanyayo Mungu itadumu milele; haiwezekani kuizidisha kitu, wala kuipunguza kitu; nayo Mungu ameifanya ili watu wamche Yeye.”

Kwa nini tunajifunza somo hili? Kujikumbusha ufupi wa siku zetu sio kitu kibaya kwani kunatupa hekima ya kujua namna ya kuishi kwa Amani na kutumia siku zetu kwa hekima tuwapo hapa duniani Zaburi 90:12 “Basi, utujulishe kuzihesabu siku zetu, Tujipatie moyo wa hekima.” Kwa hiyo somo hili lina baadhi ya mwaswala Muhimu yanayotuongoza jinsi na na mna ya kuzitumia siku zetu chache duniani kwa hekima, uchahce huu pia unachangiwa na kuwa zinapita haraka sana hata kama utaishi miaka mia, bado utaona ni kama zimepita haraka sana, Na kule kujifunza somo hili hakuna uhusiano wowote na unabii wa kifo cha mtu hapa, hapana ni kwaajili ya kuishi maisha mazuri tuwapo duniani!. Tutajifunza somo hili Mwanadamu siku zake zi kama majani kwa kuzingatia vipengele viwili vifuatavyo:-


·         Mwanadamu siku zake zi kama majani

·         Jinsi ya kutumia muda tuliopewa Duniani


Mwanadamu siku zake zi kama majani.

Moja ya mifano ya asili inayoonyesha ufupi wa maisha ya Mwanadamu ni pamoja na majani na maua katika miti na mimea ya kondeni, majani na maua huishi kwa muda mfupi sana na ndio maana utaweza kuona katika maandiko majani na maua yakitumiwa kama mfano halisi au mfano hai wa kufananisha maisha mafupi ya mwanadamu

1Petro 1:24 “Maana, Mwili wote ni kama majani, Na fahari yake yote ni kama ua la majani. Majani hukauka na ua lake huanguka;”       

Kwa msingi huo maandiko yanatumia majani na maua kama mfano wa asili wa kuonyesha kitu kinachodumu kwa muda mfupi zaidi. Kwa kiyunani kitu kinachodumu kwa muda mfupi zaidi kinaitwa Ephemeral Neno hilo Ephemeral kwa kiyunani yaani Greek ni Muunganiko wa maneno mawili EPI na HEMEROS, EPI kwa kiingereza maana yake ni Upon or For na HEMEROS kwa kiingereza maana yake ni Day kwa hiyo neno Ephemeral maana yake ni “For a day” “kwa siku tu” ikiwa na maana kitu kinachoishi kwa muda mfupi sana. Ephemeral is something that lasting for a very short time yaani ni kama mwendo wa kivuli cha jua, Kwa hiyo Ephemeral maana yake ni kitu kinachoishi kwa muda mfupi sana! Kama majani, au kama maua, na pia kinachopita kwa kasi sana kama kivuli!

Zaburi 102:11-12 “Siku zangu zi kama kivuli kilichotandaa, Nami ninanyauka kama majani. Bali Wewe, Bwana utaketi ukimiliki milele, Na kumbukumbu lako kizazi hata kizazi.”         

Ayubu 14:1-2 “Mwanadamu aliyezaliwa na mwanamke Siku zake za kuishi si nyingi, naye hujaa taabu. Yeye huchanua kama vile ua, kisha hukatwa; Hukimbia kama kivuli, wala hakai kamwe.”

Muhubiri 6:12 “Kwa maana ni nani ajuaye yaliyo mema ya mwanadamu katika maisha yake, siku zote za maisha yake ya ubatili, anayoishi kama kivuli? Kwa maana ni nani awezaye kumweleza mwanadamu mambo yatakayofuata baada yake chini ya jua?

Zaburi 39:4-6 “Bwana, unijulishe mwisho wangu, Na kiasi cha siku zangu ni kiasi gani; Nijue jinsi nilivyo dhaifu. Tazama, umefanya siku zangu kuwa mashubiri; Maisha yangu ni kama si kitu mbele zako. Kila mwanadamu, ingawa amesitawi, ni ubatili.Binadamu huenda tu huko na huko kama kivuli; Hufanya ghasia tu kwa ajili ya ubatili; Huweka akiba wala hajui ni nani atakayeichukua.”

Kwa hiyo katika mtazamo wa kifalsafa, maisha ya mwanadamu hutazamwa kuwa mafupi sana bila kujali mtu ameishi maisha ya miaka mingapi hapa duniani, hii inathibitisha ukweli ya kuwa tunapaswa kujua namna na jinsi ya kutumia wakati wetu huu mfupi tulio nao kwa busara zaidi sana tukijifunza kuacha majivuno na maringo kwa sababu zozote.

Zaburi 90:10-12 “Siku za miaka yetu ni miaka sabini, Na ikiwa tuna nguvu miaka themanini; Na kiburi chake ni taabu na ubatili, Maana chapita upesi tukatokomea mara. Ni nani aujuaye uweza wa hasira yako? Na ghadhabu yako kama ipasavyo kicho chako? Basi, utujulishe kuzihesabu siku zetu, Tujipatie moyo wa hekima.”            

Jinsi ya kutumia muda tuliopewa Duniani

Tunawezaje kutumia kwa busara muda huu mfupi sana tuliopewa duniani? Ili kutumia muda huu vema tunapaswa kufikiri katika maana nzima kuhusu maisha na kulenga kutimiza kusudi kuu la maisha tulilopewa na Mungu, Maisha ni dhamana kwa hiyo:-

1.       Ishi sawa na kusudi la Mungu - Tambua ni jambo gani la Muhimu duniani ambalo Mungu anataka ulifanye?, Mungu alikuumba ili iweje? Mungu amekuleta ufanye nini? Ukiisha kutambua simamia katika siku zako zote za kuishi, kumbuka kila mwanadamu hapa duniani ana kusudi lake ambalo Mungu amemkusudia kulifanya basi kaa katika kusudi hilo, huku ukihakikisha unadumisha uhusiano wako na Mungu mapema!

 

Mhubiri 12:1-7 “Mkumbuke Muumba wako siku za ujana wako, Kabla hazijaja siku zilizo mbaya, Wala haijakaribia miaka utakaposema, Mimi sina furaha katika hiyo.Kabla jua, na nuru, na mwezi, Na nyota, havijatiwa giza; Kabla ya kurudi mawingu baada ya mvua; Siku ile walinzi wa nyumba watakapotetema; Hapo wenye nguvu watakapojiinamisha; Na wasagao kukoma kwa kuwa ni haba; Na hao wachunguliao madirishani kutiwa giza; Na milango kufungwa katika njia kuu; Sauti ya kinu itakapokuwa ni ndogo; Na mtu kusituka kwa sauti ya ndege; Nao binti za kuimba watapunguzwa; Naam, wataogopa kilichoinuka Na vitisho vitakuwapo njiani; Na mlozi utachanua maua; Na panzi atakuwa ni mzigo mzito; Na pilipili hoho itapasuka; Maana mtu aiendea nyumba yake ya milele, Nao waombolezao wazunguka njiani. Kabla haijakatika kamba ya fedha; Au kuvunjwa bakuli la dhahabu; Au mtungi kuvunjika kisimani; Au gurudumu kuvunjika birikani; Nayo mavumbi kuirudia nchi kama yalivyokuwa, Nayo roho kumrudia Mungu aliyeitoa.”

 

Kumkumbuka Mungu maana yake ni kulitumikia kusudi la Mungu au kutumikia shauri la Mungu yaani kufanya kile ambacho Mungu amateka tukifanye katika maisha yetu na kubwa zaidi tukiwatumikia watu na kuacha alama katika maisha yao, na moyo wa Mungu baba yetu aliyetuumba. Utatufurahia

 

Matendo 13:36 “Kwa maana Daudi, akiisha kulitumikia shauri la Mungu katika kizazi chake, alilala, akawekwa pamoja na baba zake, akaona uharibifu.”

               

2.       Tengeneza mahusiano mazuri – Ni muhimu katika maisha haya kuwekeza katika mahusiano, usiwe na maadui wala uadui na mtu wala usiwe na uadui na Mungu na watu, Neno la Mungu linatutaka tuwe na mahusiano mema na watu wote lakini na Mungu pia, Neno la Mungu limekazia sana uhusiano mwema, baba zetu wa Imani Ibrahimu na Isaka na Yakobo wakati wote katika maisha yao walitafuta amani kwa bidii hata baada ya kufanya makosa makubwa sana ya kibinadamu walitafuta Amani!

 

Waebrania 12:14 “Tafuteni kwa bidii kuwa na amani na watu wote, na huo utakatifu, ambao hapana mtu atakayemwona Bwana asipokuwa nao;”

 

Marko 12:29-31 “Yesu akamjibu, Ya kwanza ndiyo hii, Sikia, Israeli, Bwana Mungu wetu ni Bwana mmoja; nawe mpende Bwana Mungu wako kwa moyo wako wote, na kwa roho yako yote, na kwa akili zako zote, na kwa nguvu zako zote. Na ya pili ndiyo hii, Mpende jirani yako kama nafsi yako. Hakuna amri nyingine iliyo kuu kuliko hizi.”               

 

1Yohana 2:9-11 “Yeye asemaye kwamba yumo nuruni, naye amchukia ndugu yake, yumo gizani hata sasa. Yeye ampendaye ndugu yake, akaa katika nuru, wala ndani yake hamna kikwazo. Bali yeye amchukiaye ndugu yake, yu katika giza, tena anakwenda katika giza, wala hajui aendako, kwa sababu giza imempofusha macho.”

 

Wekeza katika ujenzi wa uhusiano mzuri kwa familia ndugu, jamaa na marafiki na katika jamii, tengeneza mtandao mwema wa uhusiano mzuri, tia moyo watu, furahisha watu, jenga jamii, onyesha kujihusisha. Salimia majirani, jichanganye katika jamii, jihusishe katika harusi zao, kama una nafasi na katika misiba yao nafasi ikiruhusu, sema na watu vizuri, cheka na watu vizuri hata wasipokutendea mema usijali wewe tenda, cheka na wanaocheka na lia na wanaolia, usiwe na maadui, uwe rafiki wa kila mtu na wa kila rika!

 

3.       Jaa shukurani – iweni watu wa shukurani, shukuru kwa kila jambo liwe kubwa au dogo na lolote lile ambalo ulimwengu unatoa

 

1Thesalonike 5:18 “shukuruni kwa kila jambo; maana hayo ni mapenzi ya Mungu kwenu katika Kristo Yesu.”

 

Zaburi 106:1, “Haleluya. Mshukuruni Bwana kwa kuwa ni mwema, Kwa maana fadhili zake ni za milele.”           

Zaburi 100:4 “Ingieni malangoni mwake kwa kushukuru; Nyuani mwake kwa kusifu; Mshukuruni, lihimidini jina lake;”   

 

Wakolosai 3:15 “Na amani ya Kristo iamue mioyoni mwenu; ndiyo mliyoitiwa katika mwili mmoja; tena iweni watu wa shukrani.”       

 

4.       Tia moyo ustawi – wakati wote hakikisha kuwa ustawi unakuwa, yaani wakati wote ongeza maarifa, ongeza ujuzi na mbinu mbalimbali za kuhakikisha unakua katika kutafuta mbinu za kujiongeza kiimani, kiuchumi na kimaisha !

 

Luka 2:40-52 “Yule mtoto akakua, akaongezeka nguvu, amejaa hekima, na neema ya Mungu ilikuwa juu yake. Basi, wazee wake huenda Yerusalemu kila mwaka, wakati wa sikukuu ya Pasaka.Na alipopata umri wake miaka kumi na miwili, walipanda kama ilivyokuwa desturi ya sikukuu; na walipokwisha kuzitimiza siku, wakati wa kurudi kwao, yule mtoto Yesu alibaki nyuma huko Yerusalemu, na wazee wake walikuwa hawana habari. Nao wakadhani ya kuwa yumo katika msafara; wakaenenda mwendo wa kutwa, wakawa wakimtafuta katika jamaa zao na wenzao; na walipomkosa, wakarejea Yerusalemu, huku wakimtafuta. Ikawa baada ya siku tatu wakamwona hekaluni, ameketi katikati ya waalimu, akiwasikiliza na kuwauliza maswali. Nao wote waliomsikia walistaajabia fahamu zake na majibu yake. Na walipomwona walishangaa, na mama yake akamwambia, Mwanangu, mbona umetutenda hivi? Tazama, baba yako na mimi tulikuwa tukikutafuta kwa huzuni. Akawaambia, Kwani kunitafuta? Hamkujua ya kuwa imenipasa kuwamo katika nyumba ya Baba yangu? Nao hawakuelewa na neno hilo alilowaambia. Akashuka pamoja nao mpaka Nazareti, naye alikuwa akiwatii; na mamaye aliyaweka hayo yote moyoni mwake. Naye Yesu akazidi kuendelea katika hekima na kimo, akimpendeza Mungu na wanadamu.”

 

1Nyakati 4:9-10 “Naye Yabesi alikuwa mwenye heshima kuliko nduguze; na mamaye akamwita jina lake Yabesi, akisema, Ni kwa sababu nalimzaa kwa huzuni. Huyo Yabesi akamlingana Mungu wa Israeli, akisema, Lau kwamba ungenibarikia kweli kweli, na kunizidishia hozi yangu, na mkono wako ungekuwa pamoja nami, nawe ungenilinda na uovu, ili usiwe kwa huzuni yangu! Naye Mungu akamjalia hayo aliyoyaomba.”          

 

5.       Ni heri kutoa kuliko kupokea – hakikisha ya kuwa unajitoa kwaajili ya wengine, fanikisha maisha ya wengine, furahia mafanikio ya wengine, rudisha katika jamii, Kwa matendo ya ukarimu, na utu wema, weka misingi ya kudumu kuwa mwema katika jamii yako kwa kadiri Mungu alivyokubariki utakumbukwa Daima na Mungu na watu pia.

 

Matendo 20:34-35 “Ninyi wenyewe mnajua ya kuwa mikono yangu hii imetumika kwa mahitaji yangu na ya wale waliokuwa pamoja nami. Katika mambo yote nimewaonyesha ya kuwa kwa kushika kazi hivi imewapasa kuwasaidia wanyonge, na kuyakumbuka maneno ya Bwana Yesu, jinsi alivyosema mwenyewe, Ni heri kutoa kuliko kupokea.”

               

Matendo 9:36-41 “Na mwanafunzi mmoja alikuwako Yafa, jina lake Tabitha, tafsiri yake ni Dorkasi (yaani paa); mwanamke huyu alikuwa amejaa matendo mema na sadaka alizozitoa. Ikawa siku zile akaugua, akafa; hata walipokwisha kumwosha, wakamweka orofani. Na kwa kuwa mji wa Lida ulikuwa karibu na Yafa, nao wanafunzi wamesikia ya kwamba Petro yuko huko, wakatuma watu wawili kwake, kumsihi na kusema, Usikawie kuja kwetu. Petro akaondoka akafuatana nao. Alipofika, wakampeleka juu orofani wajane wote wakasimama karibu naye, wakilia na kumwonyesha zile kanzu na nguo alizozishona Dorkasi wakati ule alipokuwa pamoja nao. Petro akawatoa nje wote, akapiga magoti, akaomba, kisha akaelekea yule maiti, akanena, Tabitha, ondoka. Naye akafumbua macho yake, na alipomwona Petro akajiinua, akaketi. Akampa mkono, akamwinua; hata akiisha kuwaita wale watakatifu na wajane akamweka mbele yao, hali yu hai.”

               

Matendo 10:1-8 “Palikuwa na mtu Kaisaria, jina lake Kornelio, akida wa kikosi kilichoitwa Kiitalia, mtu mtauwa, mchaji wa Mungu, yeye na nyumba yake yote, naye alikuwa akiwapa watu sadaka nyingi, na kumwomba Mungu daima. Akaona katika maono waziwazi, kama saa tisa ya mchana, malaika wa Mungu, akimjia na kumwambia, Kornelio! Akamtazama sana, akaogopa akasema, Kuna nini, Bwana? Akamwambia, Sala zako na sadaka zako zimefika juu na kuwa ukumbusho mbele za Mungu. Sasa basi, peleka watu Yafa, ukamwite Simoni, aitwaye Petro. Yeye ni mgeni wa mtu mmoja, jina lake Simoni, mtengenezaji wa ngozi, ambaye nyumba yake iko pwani, atakuambia yakupasayo kutenda. Na yule malaika aliyesema naye akiisha kuondoka, Kornelio akawaita wawili katika watumishi wake wa nyumbani, na askari mmoja, mtu mtauwa katika wale waliomhudumia daima; na alipokwisha kuwaeleza mambo yote akawatuma kwenda Yafa.”             

 

6.       Yafikirie yaliyo juu

Ni muhimu kufikiria kuhusu mambo yajayo, yanayohusiana na uzima wa milele, hata kama tutakuwa tumebarikiwa kwa kiasi gani tukiwa hapa duniani hii isiwe sababu ya kupoteza urafiki wetu na Mungu, Mafanikio yasikutoe katika kufikiri kuhusu Mungu na maswala ya milele!, Mche Mungu, fanya kila kitu huku ukijali sana maswala ya maisha ya milele usiyapuuzikie, watu wenye akili ni wale wanaomcha Mungu!

 

Mwanzo 13:2 “Naye Abramu alikuwa ni tajiri sana kwa mifugo, kwa fedha, na kwa dhahabu.”  

 

Waebrania 11:10 “Maana alikuwa akiutazamia mji wenye misingi, ambao mwenye kuubuni na kuujenga ni Mungu.”             

 

Wakolosai 3:1-4 1. “Basi mkiwa mmefufuliwa pamoja na Kristo, yatafuteni yaliyo juu Kristo aliko, ameketi mkono wa kuume wa Mungu. Yafikirini yaliyo juu, siyo yaliyo katika nchi. Kwa maana mlikufa, na uhai wenu umefichwa pamoja na Kristo katika Mungu. Kristo atakapofunuliwa, aliye uhai wetu, ndipo na ninyi mtafunuliwa pamoja naye katika utukufu.”   

 

Yakobo 4:13-16 “Haya basi, ninyi msemao, Leo au kesho tutaingia katika mji fulani na kukaa humo mwaka mzima, na kufanya biashara na kupata faida; walakini hamjui yatakayokuwako kesho. Uzima wenu ni nini? Maana ninyi ni mvuke uonekanao kwa kitambo, kisha hutoweka. Badala ya kusema, Bwana akipenda, tutakuwa hai na kufanya hivi au hivi. Lakini sasa mwajisifu katika majivuno yenu; kujisifu kote kwa namna hii ni kubaya.”           

 

Luka 12:16-21 “Akawaambia mithali, akisema, Shamba la mtu mmoja tajiri lilikuwa limezaa sana; akaanza kuwaza moyoni mwake, akisema, Nifanyeje? Maana sina pa kuyaweka akiba mavuno yangu. Akasema, Nitafanya hivi; nitazivunja ghala zangu, nijenge nyingine kubwa zaidi, na humo nitaweka nafaka yangu yote na vitu vyangu. Kisha, nitajiambia, Ee nafsi yangu, una vitu vyema vingi ulivyojiwekea akiba kwa miaka mingi; pumzika basi, ule, unywe, ufurahi. Lakini Mungu akamwambia, Mpumbavu wewe, usiku huu wa leo wanataka roho yako! Na vitu ulivyojiwekea tayari vitakuwa vya nani? Ndivyo alivyo mtu ajiwekeaye nafsi yake akiba, asijitajirishe kwa Mungu.”

 

7.       Tunza afya yako - Ni muhimu sana pia kuhakikisha unatunza afya yako, Afya ya mwili akili na roho yako, hatuwezi kufurahia maisha yote ya kimwili na kiroho kama hatutatunza afya zetu, hili ni jambo la muhimu sana !

 

3Yohana 1:2 “Maana nalifĂ„rahi mno walipokuja ndugu na kuishuhudia kweli yako, kama uendavyo katika kweli.”                

 

1Wakorintho 6:19-20 “Au hamjui ya kuwa mwili wenu ni hekalu la Roho Mtakatifu aliye ndani yenu, mliyepewa na Mungu? Wala ninyi si mali yenu wenyewe; maana mlinunuliwa kwa thamani. Sasa basi, mtukuzeni Mungu katika miili yenu.”         

 

8.       Ishi kwa kiasi  - Maisha yanahitaji uwiano, yaani kiasi, jaribu kuweka kila kitu katika kiasi ridhika,  Neno kiasi katika maandiko ya kiingereza ni Soberly au Modarate  na katika kiyunani ni Sophronos ambalo maana yake ni Self possessed/Self control yaani kujidhibiti, au kujikana nafsi kwa hiyo ni muhimu kuwa na kiasi ni muhimu kujidhibiti, usipitilize mipaka katika kila jambo ulifanyalo

 

Tito 2:11-12 “Maana neema ya Mungu iwaokoayo wanadamu wote imefunuliwa; nayo yatufundisha kukataa ubaya na tamaa za kidunia; tupate kuishi kwa kiasi, na haki, na utauwa, katika ulimwengu huu wa sasa;”

 

Hitimisho:

 

Tukijikita katika mambo hayo hapo juu tutajikuta tunaishi katika utoshelevu, unaotengeneza maana kamili ya maisha bila kujali urefu au ufupi wa maisha yenyewe!

               

Na. Rev. Innocent Samuel Kamote

Mkuu wa wajenzi mwenye Hekima!     

Jumapili, 26 Mei 2024

Katika mlima wa Bwana itapatikana!


Mwanzo 22:13-14 “Ibrahimu akainua macho yake, akaangalia, na tazama, kondoo mume yuko nyuma yake, amenaswa pembe zake katika kichaka. Basi Ibrahimu akaenda akamtwaa huyo kondoo, akamtoa awe sadaka ya kuteketezwa badala ya mwanawe. Ibrahimu akapaita mahali hapo Yehova-yire, kama watu wasemavyo hata leo, Katika mlima wa BWANA itapatikana.”




Utangulizi:

Ni muhimu kufahamu na kujikumbusha tena na tena ya kuwa Mungu wetu ni mwaminifu na anajishughulisha sana na maisha yetu katika namna ya kushangaza sana kiasi ambacho akili zetu haziwezi kuelewa wakati mwingine, jinsi Mungu alivyo mwema katika maisha yetu, Lakini ni ukweli ulio wazi kuwa Mungu anajishughulisha sana na mambo yetu, na yeye hutupatia mahitaji yetu ya kimwili na kiroho, zaidi ya yote ni Mwalimu mzuri sana wa neno lake kivitendo. Mungu anazo njia elfu nyingi za kututunza watu wake ambazo wala hatuzijui, Endapo tu tutaamua kujiachilia kwa Mungu kwa Imani bila shaka, utamuona Mungu kama Yehova Yire katika maisha yako na hutatikisika.

1Petro 5:6-7 “Basi nyenyekeeni chini ya mkono wa Mungu ulio hodari, ili awakweze kwa wakati wake; huku mkimtwika yeye fadhaa zenu zote, kwa maana yeye hujishughulisha sana kwa mambo yenu.”

Wengi wetu tuliookolewa wakati tunapopita majaribuni, huwa tunajawa na mashaka na kuanza kuumiza vichwa kuwa mambo yatakuwaje na tunashindwa kwa namna Fulani kumpa Mungu nafasi ya kutuhudumia kwa sababu tu ya mashaka yetu, ukweli ni kuwa tukishindwa kumwachia Mungu fadhaa zetu na tukajaribu kuzibeba wenyewe tutajikuta tunashindwa na tunazimia roho na tunaweza kukosa Amani ile ambayo Mungu ameikusudia kwetu

Leo tutachukua muda kujifunza kwa kina na mapana na marefu na kumwangalia Mungu wetu kama Jehovah Yire katika somo hili Katika mlima wa Bwana itapatikana! Tutajifunza somo hili kwa kuzingatia mambo ya msingi yafuatayo:-


·         Ibrahimu katika kipimo cha juu kabisa cha Imani

·         Katika mlima wa Bwana itapatikana

·         Jinsi na namna bwana atakavyokupatia


Ibrahimu katika kipimo cha juu kabisa cha Imani

Moja ya eneo ambalo linathibitisha ukuaji wa Imani ya Ibrahimu ni mara baada ya kushinda kipimo hiki cha juu kabisa cha Imani, Mwanzo 22:1-3 “Ikawa baada ya mambo hayo Mungu alimjaribu Ibrahimu, akamwambia, Ee Ibrahimu! Naye akasema, Mimi hapa. Akasema, Umchukue mwanao, mwana wako wa pekee, umpendaye, Isaka, ukaende zako mpaka nchi ya Moria, ukamtoe sadaka ya kuteketezwa huko juu ya mlima mmojawapo nitakaokuambia. Ibrahimu akaondoka alfajiri, akatandika punda wake, akachukua vijana wawili pamoja naye, na Isaka mwanawe, akachanja kuni kwa ajili ya hiyo sadaka ya kuteketezwa, akaondoka, akaenda mpaka mahali alipoambiwa na Mungu.”

Mungu alikuwa amemjaribu Ibrahimu kwa kiwango cha juu kabisa, tena katika namna ya kushangaza sana ambayo iko kinyume na akili za kawaida za kibinadamu, na tabia na upendo wa Mungu, na zaidi ya yote kama mzazi wa Isaka, lakini katika namna ya kushangaza sana Ibrahimu alikuwa tayari kumtii Mungu katika kipimo hiki akiwa na imani kali sana, kimsingi tunaweza kusema kuwa Ibrahimu aliwahi kupimwa na Mungu katika mazingira makubwa matatu

1.       Kuondoka katika nchi yake mwenyewe na kwenda asikojua  - hii ilitokea wakati Mungu aliposema na Ibrahimu kwa mara ya kwanza kabisa kuwa aondoke katika nchi yake na nchi ya baba zake na watu wake aende katika inchi atakayoonyeeshwa na kimsingi inchi hiyo pia alikuwa hajaijua na Mungu alikuwa hajamwambia kuwa ni wapi ona

 

Mwanzo 12:1-4 “BWANA akamwambia Abramu, Toka wewe katika nchi yako, na jamaa zako, na nyumba ya baba yako, uende mpaka nchi nitakayokuonyesha; nami nitakufanya wewe kuwa taifa kubwa, na kukubariki, na kulikuza jina lako; nawe uwe baraka; nami nitawabariki wakubarikio, naye akulaaniye nitamlaani; na katika wewe jamaa zote za dunia watabarikiwa. Basi Abramu akaenda, kama BWANA alivyomwamuru; Lutu akaenda pamoja naye. Naye Abramu alikuwa mtu wa miaka sabini na mitano alipotoka Harani.”

 

Waebrania 11:8-9 “Kwa imani Ibrahimu alipoitwa aliitika, atoke aende mahali pale atakapopapata kuwa urithi; akatoka asijue aendako. Kwa imani alikaa ugenini katika ile nchi ya ahadi, kama katika nchi isiyo yake, akikaa katika hema pamoja na Isaka na Yakobo, warithi pamoja naye wa ahadi ile ile.”                

 

Katika kipimo hiki Ibrahimu alifanikiwa kwani alitii na kuondoka kwenda katika inchi aliyoahidiwa na Mungu ambayo kimsingi ilikuwa inchi ya mkanaani na Mungu alimthibitishia kuwa atampa inchi hiyo yeye na uzao wake

 

Mwanzo 17:1-9. “Abramu alipokuwa mtu wa miaka tisini na kenda, BWANA akamtokea Abramu, akamwambia, Mimi ni Mungu Mwenyezi, uende mbele yangu, ukawe mkamilifu. Nami nitafanya agano langu kati ya mimi na wewe, nami nitakuzidisha sana sana. Abramu akaanguka kifudifudi. Mungu akamwambia, akasema, Mimi, agano langu nimefanya nawe, nawe utakuwa baba wa mataifa mengi, wala jina lako hutaitwa tena Abramu, lakini jina lako litakuwa Ibrahimu, kwani nimekuweka uwe baba wa mataifa mengi. Nitakufanya uwe na uzao mwingi sana, nami nitakufanya kuwa mataifa, na wafalme watatoka kwako. Agano langu nitalifanya imara kati ya mimi na wewe, na uzao wako baada yako, na vizazi vyao, kuwa agano la milele, kwamba nitakuwa Mungu kwako na kwa uzao wako baada yako. Nami nitakupa wewe na uzao wako baada yako nchi hii unayoikaa ugeni, nchi yote ya Kanaani, kuwa milki ya milele; nami nitakuwa Mungu wao. Mungu akamwambia Ibrahimu, Nawe ulishike agano langu, wewe na uzao wako kwa vizazi vyao baada yako.”

 

2.       Jaribu la kuwa na subira -  Mungu alimuahidi Ibrahimu kuwa atampa uzao kupitia Sara mke wake wakati ahadi inatolewa Ibrahimu alikuwa na miaka 75 bila shaka Sara alikuwa na miaka 65 kwa sababu Ibrahimu na Sara walikuwa na tofauti ya miaka 10, Jaribu hili la kuwa na subira kwa kweli liliwashinda, hata na sisi tunashindwa mara nyingi sana katika eneo la kuwa na subira  wapi Mungu alimuahidi Ibrahimu mtoto ona

 

Mwanzo 18:10-13Akamwambia, Hakika nitakurudia wakati huu huu mwakani, na tazama, Sara mkeo atapata mwana wa kiume. Sara akasikia mlangoni pa hema iliyokuwapo nyuma yake. Basi Ibrahimu na Sara walikuwa wazee, na umri wao mkubwa, na Sara alikuwa amekoma katika desturi ya wanawake. Kwa hiyo Sara akacheka moyoni mwake, akisema, Niwapo mkongwe, nitapata furaha, na bwana wangu mzee? BWANA akamwambia Ibrahimu, Mbona Sara amecheka akisema, Mimi kweli nitazaa mwana, nami ni mzee?

 

Katika mtihani huu hata hivyo Sara na Ibrahimu walikosa uvumilivu, kutimia kwa ahadi hii ya Mungu kuligharimu miaka karibu 25 hivi kwa hiyo hapo katikati mambo yalikuwa tofauti na Sara alikata tamaa na Ibrahimu alikubaliana na kukata tamaa huko na wakajitafutia mtoto, kwa njia za kibinadamu na kitamaduni.

 

Mwanzo 16:1-4 “Basi Sarai mkewe Abramu hakumzalia mwana, naye alikuwa na mjakazi, Mmisri, jina lake Hajiri. Sarai akamwambia Abramu, Basi sasa, BWANA amenifunga tumbo nisizae, umwingilie mjakazi wangu labda nitapata uzao kwa yeye. Abramu akaisikiliza sauti ya Sarai. Sarai mkewe Abramu akamtwaa Hajiri Mmisri mjakazi wake, baada ya kukaa Abramu katika nchi ya Kanaani miaka kumi, akampa Abramu mumewe, awe mkewe. Basi akamwingilia Hajiri, naye akapata mimba. Naye alipoona ya kwamba amepata mimba, bibi yake alikuwa duni machoni pake.”

 

Pamoja na Sara na Ibrahimu kushindwa jaribu hili, utaweza kuona kwa kuwa Mungu ndiye aliyekuwa ameahidi, Mungu ni mwaminifu hata kama watu hawaamini yeye hubaki wa kuaminiwa 2Timotheo 2:12-13 “Kama tukistahimili, tutamiliki pamoja naye; Kama tukimkana yeye, yeye naye atatukana sisi; Kama sisi hatuamini, yeye hudumu wa kuaminiwa. Kwa maana hawezi kujikana mwenyewe.”

 

Mungu yeye aliitimiza ahadi yake na Sara na Ibrahimu walipata mtoto kama alivyosema Bwana, muda haukuwa kitu kwa Mungu lakini Muda ulisumbua wanadamu,  na unaendelea kuwasumbua wanadamu hata sasa, kwa kawaida ni ngumu kusubiri,  na kusubiri huwasumbua wanadamu

 

Mwanzo 21:1-5 BWANA akamjia Sara kama alivyonena, na BWANA akamfanyia kama alivyosema. Sara akapata mimba akamzalia Ibrahimu mwana wa kiume katika uzee wake, kwa muhula alioambiwa na Mungu. Ibrahimu akamwita jina lake Isaka, yule mwana aliyezaliwa, ambaye Sara alimzalia. Ibrahimu akamtahiri Isaka mwanawe, alipokuwa mwenye siku nane, kama Mungu alivyomwamuru. Naye Ibrahimu alikuwa mtu wa miaka mia, alipozaliwa mwana wake Isaka.”             

 

3.       Jaribu la kumtoa Isaka kama sadaka ya kuteketezwa – jaribu hili ndilo lilikuwa kipimo cha juu zaidi kwa Ibrahimu, lakini habari njema ni kuwa Ibrahimu sasa alikuwa amekuwa kiimani, sasa alijua ya kuwa Mungu akisema kitu amesema na hakuna ubabaishaji kwake, kwa hiyo Mungu aliposema naye kuhusu swala la kumtoa Isaka Imani ya Ibrahimu ilikuwa kubwa sana kwani licha ya kuwa mtihani huu ulikuwa mgumu sana kibinadamu lakini kwaajili ya uelewa wake, upendo wake na imani yake kwa Mungu. Ibrahimu alikuwa amefikia ngazi ya juu zaidi ya Imani ya kusema kuwa sasa yuko tayari kutii, huenda kushindwa kwake katika kusubiri kwa jaribu la pili kulikuwa kumemkomaza kuwa hataki tena kumkwaza Mungu kwa agizo lolote hivyo jamaa alitii ona:-

 

Mwanzo 22:1-3 “Ikawa baada ya mambo hayo Mungu alimjaribu Ibrahimu, akamwambia, Ee Ibrahimu! Naye akasema, Mimi hapa. Akasema, Umchukue mwanao, mwana wako wa pekee, umpendaye, Isaka, ukaende zako mpaka nchi ya Moria, ukamtoe sadaka ya kuteketezwa huko juu ya mlima mmojawapo nitakaokuambia. Ibrahimu akaondoka alfajiri, akatandika punda wake, akachukua vijana wawili pamoja naye, na Isaka mwanawe, akachanja kuni kwa ajili ya hiyo sadaka ya kuteketezwa, akaondoka, akaenda mpaka mahali alipoambiwa na Mungu.”

 

Tukio la utii wa Ibrahimu mahali hapa lilimpa Ibrahimu kuwa mtu mwenye heshima zaidi miongoni mwa watu ambao wamewahi kupata kumuamini Mungu, Mungu aliapa kumbariki Abrahamu kwa sababu alikuwa amekuwa kiimani, kwani alionyesha kuwa anamwamini Mungu sio tu kwa kutii agizo hilo lakini Abrahamu aliamini ya kuwa huenda hata baada ya kufanya hivyo Mungu atamfufua mwanae Isaka kutoka kwa wafu.

 

Waebrania 11:17-19 “Kwa imani Ibrahimu alipojaribiwa, akamtoa Isaka awe dhabihu; na yeye aliyezipokea hizo ahadi alikuwa akimtoa mwanawe, mzaliwa pekee; naam, yeye aliyeambiwa, Katika Isaka uzao wako utaitwa, akihesabu ya kuwa Mungu aweza kumfufua hata kutoka kuzimu; akampata tena toka huko kwa mfano.”

 

Katika kuamini na kutii agizo hili au jaribio hili la tatu kuna matukio kadhaa ya kiimani yaliyoambatana na tukio hili, tukio hili lilileta Baraka kubwa sana kwa Ibrahimu, lakini pia lilileta Baraka kubwa sana kwa ulimwengu, Ibrahimu kama nabii, na mwanae Isaka kama nabii kimsingi walitabiri ujio wa Yesu Kristo, kinabii Ibrahimu akisimama kama Mungu na Isaka akisimama kama mwana wa Mungu (Yesu Kristo) na mlima ule Moria ukisimama kama Golgotha na kuni zile zikisimama kama msalaba, ambapo Isaka anabeba kuni zile ambazo angeenda kutolewa dhabihu juu yake ni picha ya Yesu Kristo akiwa amebeba msalaba wake ambapo alikwenda kusulubiwa juu ya msalaba ule kwaajili ya ulimwengu mzima, Pamoja na somo hilo zuri jambo lingine la msingi tunalojifunza hapa ni neno lile Katika mlima wa Bwana itapatikana nini hiyo hilo linatuleta katika kutafakari kipengele cha pili.

 

Katika mlima wa Bwana itapatikana!

 

Ibrahimu na Isaka wakiwa njiani kuna maswala ya Msingi ambayo yanatufundisha na kutufunulia tabia ya Mungu tunayemuabudu kuwa ni Mungu wa namna gani, kwanza inaonekana wazi kuwa tabia ya Ibrahimu kumuabudu Mungu lilikuwa ni jambo la kawaida na huenda alikuwa amemfundisha Isaka mara kadhaa namna na jinsi anavyoendesha ibada zake, kwa hiyo Isaka katika ujana wake alikuwa amekwisha kuelewa jinsi Mungu anavyopokea dhabihu na namna dhabihu ya kuteketezwa inavyotekelezwa, Kimsingi kuwa na moto, na kuni na kisu pekee na kuelekea katika eneo la kuabudu havikuwa na msingi kama hakuna mwana kondoo, Kwa hiyo Isaka katika akili zake alifikiri kuwa safari hii baba yake atakuwa amesahahu au amepuuzia jambo la Muhimu katika ibada hiyo ambayo kimsingi ni mwana kondoo na kukaa kimya kungeweza kuwafanya waende mbali zaidi huku akiwa au wakiwa hawana kondoo wa sadaka hivyo Isaka akauliza

 

Mwanzo 22:5-8 “Ibrahimu akawaambia vijana wake, Kaeni ninyi hapa pamoja na punda, na mimi na kijana tutakwenda kule, TUKAABUDU, NA KUWARUDIA TENA. Basi Ibrahimu akazitwaa kuni za hiyo sadaka, akamtwika Isaka mwanawe; akatwaa moto na kisu mkononi mwake, wakaenda wote wawili pamoja. Isaka akasema na Ibrahimu baba yake, akinena, Babangu! Naye akasema, Mimi hapa, mwanangu. Akasema, Tazama! Moto upo, na kuni zipo, lakini yuko wapi mwana-kondoo kwa sadaka ya kuteketezwa? Ibrahimu akasema, MUNGU ATAJIPATIA MWANA-KONDOO KWA HIYO SADAKA, mwanangu. Basi wakaendelea wote wawili pamoja.”

 

Kimsingi maneno haya ya Ibrahimu yenyewe yalikuwa yamejaa Imani kubwa na unabii mkubwa na wa ajabu, Ibrahimu alikuwa amewabakiza vijana wakae na punda na kuwapa maelekezo kuwa yeye na kijana yaani Isaka watakwenda kuabudu na kisha KUWARUDIA TENA, kwa hiyo Ibrahimu alikua na uhakika kuwa atarudi na Isaka kama anavyokwenda naye, lakini jambo la pili swali la Isaka kwa baba yake kuwa moto upo, na kuni zipo lakini mwana-kondoo kwa sadaka ya kutekeketezwa yuko wapi? Ibrahimu anamjibu Isaka kuwa MUNGU ATAJIPATIA  neno hili kwa kiebrania linasomeka kama “elohiym raah” au Yehoha Yire maana yake kwa kingereza God will Provide  au Kiswahili Mungu atajipatia au katika mlima wa bwana itapatikana, kwa hiyo Isaka anapouliza sadaka iko wapi Ibrahimu anajibu katika mlima wa Bwana itapatikana  neno hili lilikuwa na maana gani?

 

Maana kubwa na ya msingi ni kuwa Mungu mwenyewe ataleta mwana kondoo sahihi kwa sadaka ya dhambi itakayowakomboa wanadamu wote, Mungu alitimiza yeye mwenyewe kile ambacho alikuwa amemuagiza Ibrahimu akifanye, kwa hiyo ni kweli Mungu aliwapa mwana kondoo aliyekuwa amenasa pembe zake katika kichaka cha miiba ikiwa ni picha ya Kristo aliyevishwa taaji ya miiba wakati anasulubiwa msalabani pale Golgotha , kauli ya Ibrahim ilitimizwa na Mungu kwa wakati ule kwa kuwapa kondoo halisi, lakini kinabii kwa Mungu kumtoa mwanakondoo atakayechukua dhambi za ulimwengu yaani Yesu Kristo

 

Mwanzo 22:9-14 “Wakafika mahali pale alipoambiwa na Mungu, Ibrahimu akajenga madhabahu huko, akaziweka tayari kuni, kisha akamfunga Isaka mwanawe, akamweka juu ya madhabahu, juu ya zile kuni. Ibrahimu akanyosha mkono wake, akakitwaa kisu ili amchinje mwanawe. Ndipo malaika wa BWANA akamwita kutoka mbinguni, akasema, Ibrahimu! Ibrahimu! Naye akasema,Mimi hapa. Akasema, Usimnyoshee kijana mkono wako, wala usimtendee neno; kwa maana sasa ninajua ya kuwa unamcha Mungu, iwapo hukunizuilia mwanao, mwanao wa pekee. Ibrahimu akainua macho yake, akaangalia, na tazama, kondoo mume yuko nyuma yake, amenaswa pembe zake katika kichaka. Basi Ibrahimu akaenda akamtwaa huyo kondoo, akamtoa awe sadaka ya kuteketezwa badala ya mwanawe. Ibrahimu akapaita mahali hapo Yehova-yire, kama watu wasemavyo hata leo, Katika mlima wa BWANA itapatikana.”

 

Yohana 1:29-32 “Siku ya pili yake amwona Yesu anakuja kwake, akasema, Tazama, Mwana-kondoo wa Mungu, aichukuaye dhambi ya ulimwengu! Huyu ndiye niliyenena habari zake ya kwamba, Yuaja mtu nyuma yangu, ambaye amekuwa mbele yangu; kwa maana alikuwa kabla yangu. Wala mimi sikumjua; lakini kusudi adhihirishwe kwa Israeli ndiyo maana mimi nalikuja nikibatiza kwa maji. Tena Yohana akashuhudia akisema, Nimemwona Roho akishuka kama hua kutoka mbinguni; naye akakaa juu yake.”

 

Kwa hiyo kimsingi, Ibrahimu alikuwa ametabiri ya kuwa Mungu atatimiza mahitaji yetu yote ya ukombozi wa mwanadamu na kutupatia wokovu, Ibrahimu alikuwa ameonyesha wazi kuwa kutakuwa na ukomo kwa sadaka za kutetekezwa pale Mungu atakapokuja kumtoa mwana wake wa pekee ambaye ndiye Yesu aliyekufa msalabani na kutuletea wokovu.

 

Jambo lingine tunalijifunza kutoka katika neno Yehova Yire yaani katika mlima wa Bwana itapatikana ni kuwa Mungu anajihusisha na mahitaji yetu sio ya kiroho tu bali na ya mwilini, Yehova yire maana yake Mungu atatoa, kila wakati tunapokuwa na upungufu wa aina yoyote katika mahitaji yetu ya mwilini ni lazima kwetu kujishusha na kumuachia Mungu na kumtazama Mungu kwa Imani kuwa atajishughulisha na mahitaji yetu, tunapokuwa tumepungukiwa na kitu Mungu wetu alituahidi ya kuwa hatatupungukia wala hatatuacha, Mungu atatupima Imani yetu kwa kutupitisha jangwani, atatupima Imani yetu tunapokuwa hatuna kazi, atatupima Imani yetu tunapokuwa hatuna chakula, hatuna fedha za kulipa bili ya umeme,  au ya maji, au kodi ya nyumba, au nauli ya dala dala, na wakati mwingine hata sadaka ya kumtolea yeye, au tunadaiwa kila kona jiachilie katika Mungu mwamini Mungu ya kuwa atashughulika na mahitaji yako kwa sababu yeye ni Yehova yire na katika mlima wake itapatikana! Ikiwa tuna mahitaji yoyote ya kimwili na kiroho, tunahitaji uwepo wake, tunahitaji neema yake au huruma zake yeye yupo na tunapomwangalia yeye atatupatia hata baada ya kupitia njia ya mateso, hofu na mashaka yakuwa itajuwaje Yeye atatupa uwepo wake na nguvu zake zitadhihirika na sisi tutakuwa katika Imani kwa msaada wa Mungu wetu Haleluyaa!                          

Jinsi na namna Bwana atakavyokupatia

Inawezeakana unakutana na somo hili ukiwa huelewi kuwa utatoka vipi katika hali unayoipitia, hujui itakuwaje, huna wa kukutia moyo, kutokana na magumu unayokutana nayo, huna fedha, huna namna ya kujitibu, kihisia hakuko vema, umejawa na mashaka na wasiwasi, majaribu yamekuzunguka kila kona, ni kama umepoteza tumaini, unahangaika, hakuna anayekujali, kuna mambo chungu nzima yanasumbua kichwa chako, hujui kesho itakuwaje, ada ya watoto shule itakuwa vipi, wazazi wanaokutegemea utawatunza vipi, ndugu zako uliokuwa unawasaidia, utawasaidiaje, mbingu ni kama zimekuwa chuma na ardhi ni kama imekuwa shaba, shambani mambo yamekataa, miradi imegoma, mzunguko wa fedha ni kama hauko, biashara haziendi, unawaza hivi itapatikana? Ndoa itapatikana? Kazi itapatikana? Uamsho kanisani kwangu utapatikana? Mtoto atapatikana? Mavazi yatapatikana ?, washirika katika huduma yangu watapatikana? Sadaka katika wakati huu mgumu itapatikana?  Endapo unazungukwa na maswali mengi sana yanayofanana na hayo somo hili haliko mikononi mwako kwa bahati Mbaya Roho Mtakatifu alinitaka niliandae somo hili na aliniambia nilimalize mara moja, nilikuwa na masomo mengine naendelea nayo, lakini niliamuriwa niayaache nishughulike na hili kwaajili yako wewe unayesoma somo hili Bwana anakuambia leo katika mlima wa Bwana itapatikana na unaweza kuniuliza swali itapatikanaje? Kumbuka Ibrahimu hakuwa na mahali aliponukuu ahadi ya Mungu au neno la Mungu ya kuwa Mungu ni Yehova Yire wala hakuwa na mahali pameandikwa katika mlima wa bwana itapatikana lakini Isaka alipouliza, Ibrahimu alijibu moja kwa moja kama vile vile Mungu alivyomfanyia baadaye nasema katika mlima wa bwana itapatikana, itapatikanaje sisi tunazo ahadi za Mungu nyingi sana zinazoonyesha kuwa Mungu anashughulika na mahitaji yetu

a.       Anashughulika na mahitaji yetu ya mwilini – Mungu aliyetuumba anatujua sisi ni viumbe wake na alipotuumba aliandaa kila kitu kwaajili yetu, anawajibika kutulisha kama anavyolisha wanyama na ndege wa angani kwa hiyo Mungu wetu hashindwi kujitokeza katika mahitaji yetu yote na katika chakula

Wafilipi 4:19 “Na Mungu wangu atawajazeni kila mnachokihitaji kwa kadiri ya utajiri wake, katika utukufu, ndani ya Kristo Yesu.”

Luka 12:240-26 “Watafakarini kunguru, ya kwamba hawapandi wala hawavuni; hawana ghala wala uchaga, na Mungu huwalisha. Bora ninyi mara nyingi kuliko ndege! Na yupi kwenu ambaye akijisumbua aweza kujiongeza kimo chake hata mkono mmoja? Basi, ikiwa hamwezi hata neno lililo dogo, kwa nini kujisumbua kwa ajili ya yale mengine?

Zaburi 145:14-16 “Bwana huwategemeza wote waangukao, Huwainua wote walioinama chini.Macho ya watu wote yakuelekea Wewe, Nawe huwapa chakula chao wakati wake. Waufumbua mkono wako, Wakishibisha kila kilicho hai matakwa yake.”

Zaburi 37:25 “Nalikuwa kijana nami sasa ni mzee, Lakini sijamwona mwenye haki ameachwa Wala mzao wake akiomba chakula.”

b.      Mungu atakupa pumziko – Yesu/Mungu ameahidi kutupa pumziko, najua unahangaika sana roho yako inatanga tanga, hata wale waliokutimua wanataka kujua itakuwaje, wanatamani kujua unaishije, wanataka kuona ukihangaika, wanatamani kuona ukienda kuwaomba na kuwakopa, au ukihangaika, moyo wako ni kama una hofu hivi lakini weka tumaini lako kwa Yesu nawe utapata Pumziko.

 

Mathayo 11:28-29 “Njoni kwangu, ninyi nyote msumbukao na wenye kulemewa na mizigo, nami nitawapumzisha. Jitieni nira yangu, mjifunze kwangu; kwa kuwa mimi ni mpole na mnyenyekevu wa moyo; nanyi mtapata raha nafsini mwenu;”

 

Zaburi 23:1-6 “Bwana ndiye mchungaji wangu, Sitapungukiwa na kitu. Katika malisho ya majani mabichi hunilaza, Kando ya maji ya utulivu huniongoza. Hunihuisha nafsi yangu; na kuniongoza Katika njia za haki kwa ajili ya jina lake.Naam, nijapopita kati ya bonde la uvuli wa mauti, Sitaogopa mabaya; Kwa maana Wewe upo pamoja nami, Gongo lako na fimbo yako vyanifariji.Waandaa meza mbele yangu, Machoni pa watesi wangu. Umenipaka mafuta kichwani pangu, Na kikombe changu kinafurika. Hakika wema na fadhili zitanifuata Siku zote za maisha yangu; Nami nitakaa nyumbani mwa Bwana milele.”

 

c.       Mungu atakupa muongozo - Ni kazi ya Mungu kutuongoza na kutusafishia njia kwaajili ya kusudi lake, wakati mwingine unapokuwa na mashaka kuhusu muelekeo unawaza itapatikana kweli? Kuna muelekeo kweli yuko anayetoa muelekeo na atakuongoza kwenye maji ya utulivu, kwa nini kwa sababu anatoa muongozo, watu wengine hawawezi kujua njia yetu kwa sababu wao sio Mungu, wanadamu wakiijua njia yako wanaweza kuiharibu lakini Mungu ndiye mwenye mwenendo na yeye ndiye njia.

 

Mithali 3:5-6 “Mtumaini Bwana kwa moyo wako wote, Wala usizitegemee akili zako mwenyewe; Katika njia zako zote mkiri yeye, Naye atayanyosha mapito yako.”

 

Mithali 20:24 “Mwenendo wa mtu watoka kwa Bwana; Basi, awezaje mtu kuelewa na njia yake?

 

Zaburi 37:5-6 “Umkabidhi Bwana njia yako, Pia umtumaini, naye atafanya. Ataitokeza haki yako kama nuru, Na hukumu yako kama adhuhuri

 

d.      Mungu atatuoa neema – Iko neema maalumu ambayo Mungu atatupa kwaajili ya kila aina ya mapito unayoyapitia, neema ya Mungu itatuisaidia, itatusaidia kuwasamehe waliotukosea, na kusahau yote, itatusaidia kufurahi katika mazingira ambayo tulitakiwa tuwe tunalia, itatusaidia kuwapa kipaumbele wenzetu katika ndoa, itatusaidia kuzitunza familia zetu, neema itarahisisha maisha na kutupa nguvu ya kusonga mbele katika namna ya kushangaza sana, neema ya Mungu hainunuliwi, neema ya Mungu haipatikani kwa kujipendekeza, neema ya Mungu inatolewa Bure na kutufaa wakati wa mahitaji, Yeye mwenyewe anatoa, Mungu mwenyewe atatupa neema ya kuitusaidia wakati wa mahitaji yetu!

 

Waebrania 4:15-6. “Kwa kuwa hamna kuhani mkuu asiyeweza kuchukuana nasi katika mambo yetu ya udhaifu; bali yeye alijaribiwa sawasawa na sisi katika mambo yote, bila kufanya dhambi. Basi na tukikaribie kiti cha neema kwa ujasiri, ili tupewe rehema, na kupata neema ya kutusaidia wakati wa mahitaji.”

 

2Wakorintho 9:8 “Na Mungu aweza kuwajaza kila neema kwa wingi, ili ninyi, mkiwa na riziki za kila namna siku zote, mpate kuzidi sana katika kila tendo jema;”

 

Shetani na maajenti wake na maadui wanaotutakia mabaya hawajui kuwa iko neema na rehema za kutusaidia wakati wa mahitaji yetu, Mungu hujalia neema hiyo, Paulo alipokuwa na uhitaji wa kile alichokiita mwiba katika maisha yake Mungu alimjibu kuwa neema inatosha, maana yake Mungu akitupa neema yake tunawezeshwa kustahimili yale yanayotusibu kwa Amani bila kukosana na Mungu wetu wala kuwaudhi watu omba neema ya Mungu siku zote katika maisha yako na utakuwa na Amani kwani neema yake itakubeba.

 

e.      Mungu atatupa njia ya kutokea – Ni Isaka aliyekuwa amefungwa mikono yake, ni Isaka aliyekuwa katika hatari ya kuchomwa kisu na baba yake, wakati anasumbuka yuko wapi mwana kondoo, ghafla anashangaa kumbe yeye ndiye anayefanywa kondoo siku ile? Najua umefanywa kondoo wa kafara mara kadhaa katika maisha yako, watu waliona wakutoe wewe, ili wapate nafuu, waliona ufukuzwe wewe, waliona wakusingizie wewe, waliona wakuharibie wewe lakini kama alivyosema Ibrahimu Katika mlima wa Mungu itapatikana maana yake Mungu atajipatia mwana kondoo, kwa kila jaribu unalolipitia bwana ataweka na mlango wa kutokea.

 

Mwanzo 22:9-13 “Wakafika mahali pale alipoambiwa na Mungu, Ibrahimu akajenga madhabahu huko, akaziweka tayari kuni, kisha akamfunga Isaka mwanawe, akamweka juu ya madhabahu, juu ya zile kuni. Ibrahimu akanyosha mkono wake, akakitwaa kisu ili amchinje mwanawe. Ndipo malaika wa BWANA akamwita kutoka mbinguni, akasema, Ibrahimu! Ibrahimu! Naye akasema, Mimi hapa. Akasema, Usimnyoshee kijana mkono wako, wala usimtendee neno; kwa maana sasa ninajua ya kuwa unamcha Mungu, iwapo hukunizuilia mwanao, mwanao wa pekee. Ibrahimu akainua macho yake, akaangalia, na tazama, kondoo mume yuko nyuma yake, amenaswa pembe zake katika kichaka. Basi Ibrahimu akaenda akamtwaa huyo kondoo, akamtoa awe sadaka ya kuteketezwa badala ya mwanawe.”

 

1Wakorintho 10:13Jaribu halikuwapata ninyi, isipokuwa lililo kawaida ya wanadamu; ila Mungu ni mwaminifu; ambaye hatawaacha mjaribiwe kupita mwezavyo; lakini pamoja na lile jaribu atafanya na mlango wa kutokea, ili mweze kustahimili.”

 

Mungu atatupatia njia ya kutoka au kulishinda jaribu linalotukumba, neema ya Mungu ilivyo njema tuna neno lake, tuna Roho wake tukisimama karibu naye na kuomba msaada wake nakuhakikishia tutaona njia mbadala.

 

f.        Mungu ataleta msaada wakati tunaumizwa au tunakaribia kuumizwa – wakati wote Mungu wetu hatakubali uonevu, na tunapoumizwa na yeyote yule hata awe mtu wa Mungu, hiyo haimaanishi kuwa Mungu hatashughulika na sisi, Yeye ni msaada uonekanao tele wakati wa mateso, wakati maumivu yanapokuwa magumu kubeba kumbuka tumkimbilie Mungu yeye sio Mungu aliye mbali, wakati Ibrahimu anakaribia kumuumiza Isaka Mungu alimtuma malaika wake mbingu ziliingilia kati.

 

Zaburi 46:1-3 “Mungu kwetu sisi ni kimbilio na nguvu, Msaada utakaoonekana tele wakati wa mateso.Kwa hiyo hatutaogopa ijapobadilika nchi, Ijapotetemeka milima moyoni mwa bahari. Maji yake yajapovuma na kuumuka, Ijapopepesuka milima kwa kiburi chake.”

 

Zaburi 34:17-19 “Walilia, naye Bwana akasikia, Akawaponya na taabu zao zote. Bwana yu karibu nao waliovunjika moyo, Na waliopondeka roho huwaokoa. Mateso ya mwenye haki ni mengi, Lakini Bwana humponya nayo yote.”

 

Mwanzo 16:6-11. “Naye Abramu akamwambia Sarai, Tazama, mjakazi wako yu mkononi mwako, mtendee lililo jema machoni pako. Sarai akamtesa, naye akakimbia kutoka mbele yake. Malaika wa BWANA akamwona kwenye chemchemi ya maji katika jangwa, chemchemi iliyoko katika njia ya kuendea Shuri. Akamwambia, Hajiri, wewe mjakazi wa Sarai, unatoka wapi, nawe unakwenda wapi? Akanena, Nakimbia mimi kutoka mbele ya bibi yangu Sarai. Malaika wa BWANA akamwambia, Rudi kwa bibi yako, ukanyenyekee chini ya mikono yake. Malaika wa BWANA akamwambia, Hakika nitauzidisha uzao wako, wala hautahesabika kwa jinsi utakavyokuwa mwingi. Malaika wa BWANA akamwambia, Tazama! Wewe una mimba, utazaa mwana wa kiume, nawe utamwita jina lake Ishmaeli, maana BWANA amesikia kilio cha mateso yako.”        

 

g.       Mungu atakupa Amani – unaonaje katika jaribu lile la Ibrahimu kama angemuua mwanae? Hata kama Mungu angemfufua katika wafu, uhusiano wa mtoto na baba yake ungekuwa mashakani, kila mmoja angepoteza Amani, lakini njia ya Mungu katika mlima wake ilikuwa ya kupendeza sana walirudi kwa Amani,  Mungu hutupoa Amani katika mazingira yoyote yale, ataitunza mioyo yetu na akili zetu zisiumizwe vibaya, anatuleta katika Amani, anatoa Amani,

 

Wafilipi 4:6-7 “Msijisumbue kwa neno lo lote; bali katika kila neno kwa kusali na kuomba, pamoja na kushukuru, haja zenu na zijulikane na Mungu. Na amani ya Mungu, ipitayo akili zote, itawahifadhi mioyo yenu na nia zenu katika Kristo Yesu.”       

 

Warumi 5:1 “Basi tukiisha kuhesabiwa haki itokayo katika imani, na mwe na amani kwa Mungu, kwa njia ya Bwana wetu Yesu Kristo, ambaye kwa yeye tumepata kwa njia ya imani kuifikia neema hii ambayo mnasimama ndani yake; na kufurahi katika tumaini la utukufu wa Mungu. Wala si hivyo tu, ila na mfurahi katika dhiki pia; mkijua ya kuwa dhiki, kazi yake ni kuleta saburi; na kazi ya saburi ni uthabiti wa moyo; na kazi ya uthabiti wa moyo ni tumaini; ”

 

h.      Mungu atakuokoa – unaweza kusema mbona nimeshaokoka lakini neno wokovu katika lugha ya kiyunani wanatumie neno Sƍtēria ambalo lina maana pana zaidi ya kusamehewa dhambi au kuzaliwa mara ya pili, Soteria ni kuwekwa huru, kuokolewa hatarini, kulindwa na hatari, kwa hiyo wakati unapitia changamoto na majaribu ya aina mbalimbali kumbuka pia kuwa Mungu atakuokoa, kama alivyomuokoa Isaka au alivyomfufua Yesu baada ya kusulubiwa Msalabani akamuokoa na mauti basi Mungu atakuokoa na wewe katika mapito yako  na hatari zako zote na maumivu yako yote.

 

Zaburi 61:1-3 “Ee Mungu, ukisikie kilio changu, Uyasikilize maombi yangu. Toka mwisho wa nchi nitakulilia nikizimia moyo, Uniongoze juu ya mwamba nisioweza kuupanda. Kwa maana ulikuwa kimbilio langu, Ngome yenye nguvu adui asinipate.”

 

Zaburi 27:1-3 “Bwana ni nuru yangu na wokovu wangu, Nimwogope nani? Bwana ni ngome ya uzima wangu, Nimhofu nani? Watenda mabaya waliponikaribia, Wanile nyama yangu, Watesi wangu na adui zangu, Walijikwaa wakaanguka. Jeshi lijapojipanga kupigana nami, Moyo wangu hautaogopa. Vita vijaponitokea, Hata hapo nitatumaini.”

Unaweza kuona Mungu ametuahidi katika neno lake kukutana na mahitaji yetu yote, wakati tunapopungukiwa anatukumbusha tu kuwa tumuamini yeye kwani Yeye kama YEHOVA YIRE  “God will provide” maana yake atakutana na mahitaji yetu na katika mlima wake itapatikana, Mungu atatoa msaada na atatupa njia na namna ya kujikwamua kutoka katika pito lako, haijalishi unapitia pito la namna gani,  fahamu tu ya kuwa Mungu amekwisha kutupa njia ya kufanya wakati wa mahitaji yetu ya kimiwli na kiroho, tunaweza kuwa na amani na utulivu tukijua ya kuwa KATIKA MLIMA WA BWANA ITAPATIKANA.

Na. Rev. Innocent Samuel Kamote

Mkuu wa wajenzi mwenye hekima!

Jumapili, 19 Mei 2024

Roho wa Bwana na Nguvu za uonevu!


Matendo 10:38 “habari za Yesu wa Nazareti, jinsi Mungu alivyomtia mafuta kwa Roho Mtakatifu na nguvu naye akazunguka huko na huko, akitenda kazi njema na kuponya wote walioonewa na Ibilisi; kwa maana Mungu alikuwa pamoja naye


Utangulizi:

Leo ni siku ya Pentecost: Pentecost ni siku ambayo wakristo duniani wanaadhimisha na kukumbuka siku ya kushuka maalumu duniani kwa ROHO MTAKATIFU  na kuanza kufanya kazi akiwa na mitume na wanafunzi wengine wa Yesu Kristo, tukio hilo maalumu limeelezwa katika kitabu cha Matendo

Matendo 2:1-4 “Hata ilipotimia siku ya Pentekoste walikuwako wote mahali pamoja. Kukaja ghafula toka mbinguni uvumi kama uvumi wa upepo wa nguvu ukienda kasi, ukaijaza nyumba yote waliyokuwa wameketi. Kukawatokea ndimi zilizogawanyikana, kama ndimi za moto uliowakalia kila mmoja wao. Wote wakajazwa Roho Mtakatifu, wakaanza kusema kwa lugha nyingine, kama Roho alivyowajalia kutamka.”

Sikukuu ya Pentecost iliadhimishwa siku ya 50 baada ya sikukuu ya Pasaka, Na neno hilo Pentecost limetokana na neno la asili ya kigiriki Pentecost ambalo maana yake ni 50, hata hivyo sikukuu ya Pentekoste ambayo huadhimishwa siku 50 baada ya pasaka au jumapili saba baada ya pasaka kwa wayahudi sikukuu hii huitwa SHAVUOT  ambayo kimsingi ilikuwa sikukuu ya mavuno kwa Wayahudi, Hata hivyo katika siku hiyo Mungu aliitumia kumuachilia Roho wake Mtakatifu kuchukua nafasi na kuleta nguvu kwa wanafunzi wa Yesu ili waweze kuwa mashahidi wake na kuihubiri injili ya utukufu wa Mungu duniani kwa gharama yoyote. Siku hii huadhimishwa na njia mbalimbali na kwa hutuba mbalimbali, wengine wakiliita juma la Roho Mtakatifu, na kadhalika, Hata hivyo kwa upande wangu Roho Mtakatifu alinitaka niikumbushe jamii kuwa Roho Mtakatifu vile vile yuko kwaajili ya kushughulika na uonevu wa kila aina duniani kupitia kanisa lake, maana yake ni kuwa Roho Mtakatifu anapokuja juu ya watumishi wake na kuwapaka mafuta ni Dhahiri kuwa anawataka watumishi wake wakashughulikie uonevu na kuwaweka huru watu wake kutoka katika migandamizo ya aina mbalimbali kama vile alivyoshuka juu ya Masihi.          

Luka 4:17-19. “Akapewa chuo cha nabii Isaya, akakifungua chuo, akatafuta mahali palipoandikwa, Roho wa Bwana yu juu yangu, Kwa maana amenitia mafuta kuwahubiri maskini habari njema. Amenituma kuwatangazia wafungwa kufunguliwa kwao, Na vipofu kupata kuona tena, Kuwaacha huru waliosetwa, Na kutangaza mwaka wa Bwana uliokubaliwa.”

Kwa msingi huo leo tutachukua muda kujifunza somo hili muhimu ROHO WA BWANA NA NGUVU ZA UONEVU! na tutajifunza somo hili muhimu kwa kuzingatia vipengele kadhaa vifuatavyo:-

 

·         Maana ya  neno uonevu

·         Jinsi Mungu anavyochukizwa na uonevu

·         Roho wa Bwana na nguvu za uonevu

 

Maana ya neno uonevu.

Matendo 10:38 “habari za Yesu wa Nazareti, jinsi Mungu alivyomtia mafuta kwa Roho Mtakatifu na nguvu naye akazunguka huko na huko, akitenda kazi njema na KUPONYA WOTE WALIOONEWA na Ibilisi; kwa maana Mungu alikuwa pamoja naye

Ni muhimu kufahamu kuwa katika Biblia ya kiingereza neno na KUPONYA WOTE WALIOONEWA linasomeka  and HEALING ALL THAT WERE OPPRESSED  neno hilo walioonewa ambalo kwa kiingereza oppressed katika maandiko ya kiyunani linasomeka kama  katadunasteuƍ ambalo kwa tafasiri ya kiingereza ni exericise Dominion against,  kwa Kiswahili kutawala kwa mabavu, au kuonea kwa nguvu, kutawala kikatili, au Dhuluma. Ukatili huo unaweza kuhusisha kuchukua kitu kwa nguvu, kutumikishwa kwa ujira mdogo, kutawaliwa kimabavu, kukandamizwa, kudhulumiwa, kuteswa, kufanyishwa kazi kupita kawaida au zaidi ya muda wa kawaida, kuwekwa katika hali ya kukosa maamuzi yako mwenyewe, kuwekwa chini ya utawala wa taifa jingine, na kadhalika na kwa sababu hiyo mtu anayeonewa anajisikia uonyonge, anaugua au kulia au kuomboleza, au kukata tamaa moyoni, au kulalamika huku mtu huyo au watu hao wakiwa hawana msaada wa kujitoa katika uonevu huo. Isipokuwa kwa msaada token je yake

Kwa hiyo mojawapo ya kazi za Roho Mtakatifu ni pamoja na kuharibu nguvu za uonevu, kwa hiyo Mungu anapotaka kushughulika na uonevu wakati wowote, lazima atamtumia mtu na kumpaka mafuta mtu huyo ili aweze kushughulikia uonevuo huo,  na ndio maana Leo au katika sikukuu ya Pentekoste ya Mwaka huu tunataka kumwangalia Roho Mtakatifu katika picha kukomesha uonevu!

Luka 4:17-19. “Akapewa chuo cha nabii Isaya, akakifungua chuo, akatafuta mahali palipoandikwa, Roho wa Bwana yu juu yangu, Kwa maana amenitia mafuta kuwahubiri maskini habari njema. Amenituma kuwatangazia wafungwa kufunguliwa kwao, Na vipofu kupata kuona tena, KUWAACHA HURU WALIOSETWA, Na kutangaza mwaka wa Bwana uliokubaliwa.” Unaweza kuona katika kifungu hiki pia kiingereza cha ESV kinasomeka “to set liberty those who are oppressed”

Kwa hiyo bado tunapata picha kuwa kusudi kuu la Roho Mtakatifu kuwapa nguvu watumishi wake kwa kuwapaka mafuta kusudi kubwa ni kukomesha uonevu, Dunia imejawa na uonevu wa kila aina kutoka kwa shetani na maajenti wake, na magonjwa ni sehemu ya uonevu huo, maendeleo ya kisayansi na teknolojia hayatoshi peke yake kumuweka huru mwanadamu kutoka katika uonevu huo, aidha nguvu za kipepo kila wakati zinawasukuma wanadamu kufanya yale wasiyopenda kuyafanya hasa kuyafanya mapenzi ya Mungu,  ili kwa njia hiyo shetani apate kibali cha kuendelea kuwaonea watu na kuwakandamiza, ni makusudi basi Pentekoste hii tukajikumbusha sio tu kule kujazwa na Roho Mtakatifu na nguvu zake na kufurahia kunena kwa lugha lakini wakati huu, tukubali nguvu za Roho Mtakatifu zituelekeze katika matumizi ya kushughulika na nguvu za uonevu, maana yake nini kuelekeza nguvu zetu zote katika kufunguliwa kwa aina binadamu ambao wanaonewa na ibilisi, hii ikienda sambaba na kazi ya kuihubiri injili.

Jinsi Mungu anavyochukizwa na uonevu

Neno la Mungu linatudhihirishia kuwa Mungu anachukizwa sana na uonevu wa kila aina duniani, wakati Israel wanateswa kule Misri na wakawa wanakandamizwa katika utumwa mzito kiasi cha kulia Machozi, Mungu aliguswa na kuamua kushuka ili ashughulike na uonevu uliokuwa unaendelea wamisri wakiwaonea wana wa Israel

Kutoka 3:7-9 “BWANA akasema, Hakika nimeyaona mateso ya watu wangu walioko Misri, nami nimekisikia kilio chao kwa sababu ya wasimamizi wao; maana nayajua maumivu yao; nami nimeshuka ili niwaokoe na mikono ya Wamisri, niwapandishe kutoka nchi ile, hata nchi njema, kisha pana; nchi ijaayo maziwa na asali; hata mahali pa Mkanaani, na Mhiti, na Mwamori, na Mperizi, na Mhivi, na Myebusi. Basi, tazama, kilio cha wana wa Israeli kimenifikilia; tena nimeyaona hayo mateso ambayo Wamisri wanawatesa.”

Kumbukumbu 26:6-9 “Wamisri wakatuonea, wakatutesa, wakatutumikisha utumwa mzito. Tukamlilia Bwana, Mungu wa baba zetu; Bwana akasikia sauti yetu, akaona na taabu yetu, na kazi yetu, na kuonewa kwetu. Bwana akatutoa kutoka Misri kwa mkono wa nguvu, na kwa mkono ulionyoshwa, na kwa utisho mwingi, na kwa ishara, na kwa maajabu; naye ametuingiza mahali hapa, na kutupa nchi hii, nchi ijaayo maziwa na asali.”

Aidha kwa sababu Mungu alichukizwa na uonevu waliotendewa wana wa Israel kule Misri, aliwaonya waache kuonea watu hata wageni akiwakumbusha kuwa na wao walikuwa wageni katika inchi ya Misri, Neno hili sio kwaajili ya Israel pekee leo, lakini linamuhusu kila mmoja wetu kwamba kupitia kitabu hiki cha Musa (Torati) tunawekewa msingi wa kutokuwaonea watu wengine na kutujulisha kuwa Mungu anachukizwa na uonevu na wakati mwingine ataingilia kati kuhakikisha kuwa anawatoa watu wake kutoka katika mateso na uonevu.

Kutoka 22:21-24 “Usimwonee mgeni, wala kumtendea jeuri; kwa kuwa ninyi mlikuwa wageni katika nchi ya Misri. Usimtese mjane ye yote aliyefiwa na mumewe, wala mtoto yatima. Ukiwatesa watu hao katika neno lo lote, nao wakanililia mimi, hakika yangu nitasikia kilio chao, na hasira yangu itawaka moto, nami nitawaua ninyi kwa upanga; na wake wenu watakuwa wajane, na watoto wenu mayatima.”

Kutoka 23:9 “Usimwonee mgeni; maana, ninyi mwajua moyo wa mgeni ulivyo, kwa kuwa ninyi mlikuwa wageni katika nchi ya Misri.”

Waamuzi 10:11-12 “Naye Bwana akawaambia wana wa Israeli, Je! Sikuwaokoa ninyi na hao Wamisri, na Waamori, na wana wa Amoni, na Wafilisti? Hao Wasidoni nao, na Waamaleki, na Wamaoni, waliwaonea, nanyi mlinililia, nami niliwaokoa na mikono yao.”

Tumeona namna na jinsi ambavyo Mungu anachukizwa na uonevu, uonevu katika mazingira mbalimbali na kila eneo, iwe dhuluma, kuonea masikini, kunyanyasa wanyonge, kuwaonea wajane na yatima, na kuwaonea wageni, na kadhalika haya yote Mungu ameayaamrisha katika neno lake kuwa anachukizwa nayo, anachukizwa na ukoloni, anachukizwa na unyonyaji, anachukizwa na biashara ya utumwa, na mtu mwenye nguvu kumuonea mnyonge na hata taifa moja kulionea taifa lingine, Israel walipoonewa na wamisri, waamori, wana wa Amoni na hata wafilisti na mataifa mengine Mungu alichukizwa na kuingilia kati kukomesha uonevu huo, lakini sio hivyo tu Mungu vile vile anachukizwa na uonevu unaofanywa na shetani na mapepo yake, na zaidi sana anachukizwa na uonevu wa magonjwa na kadhalika sasa ni jinsi gani Mungu anajihusisha na kukomesha uonevu?  Neno la Mungu linatuonyesha wazi kuwa kila wakati Mungu alipotaka kukomesha uonevu aliliacha swala hilo Kwa Mungu Roho Mtakatifu, na ndipo unapoweza kuona Roho wa Mungu akitoa nguvu ya kukomesha uonevu. Roho Mtakatifu alishusha nguvu zake na kuchochea wivu kwa watumishi wake na kuwataharakisha ili kuwakomboa watu wake, hii ni ishara ya wazi kuwa Mungu hawezi kuvumilia dhuluma na uonevu.

Yeremiah 21:12 “Ee nyumba ya Daudi, Bwana asema hivi, Hukumuni hukumu ya haki asubuhi, mkawaponye waliotekwa nyara na mkono wake aliyewadhulumu, ghadhabu yangu isije ikatoka kama moto, ikaunguza, asiweze mtu ye yote kuuzima, kwa sababu ya uovu wa matendo yenu.”

Roho wa Bwana  na Nguvu ya uonevu.

Kama jinsi ambavyo tumejifunza tangu mwanzo ya kuwa Mungu anachukizwa na uonevu, na watu wake wanapougua na kulia kwaajili ya uonevu wa aina yoyote Mungu alikuwa tayari kuwainua wasaidizi, au watumishi wake au waamuzi ambao aliwapaka mafuta yaani aliwapa nguvu za Roho wake Mtakatifu kwa kusudi la kuwaokoa na adui zao waliowaonea, Mungu alifanya hivyo kila wakati, na kitabu cha waamuzi ni mojawapo ya mfano mzuri wa utendaji wa Mungu dhidi ya uonevu

Waamuzi 2:18. “Na wakati Bwana alipowainulia waamuzi, ndipo Bwana alikuwa pamoja na mwamuzi huyo, akawaokoa na mikono ya adui zao siku zote za mwamuzi huyo; maana Bwana alighairi kwa ajili ya kuugua kwao kwa sababu ya watu wale waliowaonea na kuwasumbua.

Waamuzi walipoinuliwa na Mungu waliweza kuwaokoa wana wa Israel kutoka katika mikono ya adui zao na kuwasababishia Amani na utulivu, lakini waamuzi hao hawakuenda kwa nguvu zao wenyewe bali wakati wote walipakwa mafuta na Roho Mtakatifu na kupewa nguvu ili kukomesha nguvu ya uonevu, hata kama wakati mwingine uonevu huo ulisababishwa na makossa na dhambi ya Israel wenyewe, lakini kila walipomlilia alinuka kuwasaidia

-          Wakati wa uonevu wa Kushanrishathaimu  mfalme wa Mesopotamia  aliwaonea Israel na kuwakandamiza katika utumwa mzito na Israel wakawa watumwa wake kwa miaka nane mpaka walipolia na kuugua mbele za Mungu, Na Mungu aliwainulia Mwamuzi aliyeitwa Othiniel ambaye hakwenda vitani hivi hivi bali alijiwa na Roho wa Bwana ona:-

 

Waamuzi 3:7-11 “Wana wa Israeli walifanya yaliyo maovu mbele za macho ya Bwana, nao wakamsahau Bwana, Mungu wao, nao wakawatumikia Mabaali na Maashtorethi. Kwa hiyo hasira za Bwana ziliwaka juu ya Israeli, naye akawauza na kuwatia mikononi mwa Kushan-rishathaimu mfalme wa Mesopotamia; na wana wa Israeli wakamtumikia huyo Kushan-rishathaimu muda wa miaka minane. Kisha wana wa Israeli walipomlingana Bwana, Bwana akawainulia wana wa Israeli mwokozi, aliyewaokoa, yaani, Othnieli mwana wa Kenazi, ndugu mdogo wa Kalebu. Roho ya Bwana ikamjilia juu yake, naye akawa mwamuzi wa Israeli; akatoka kwenenda vitani, naye Bwana akamtia huyo Kushan-rishathaimu, mfalme wa Mesopotamia, mkononi mwake; na mkono wake ukamshinda Kushan-rishathaimu. Nayo nchi ikawa na amani muda wa miaka arobaini. Kisha Othnieli, mwana wa Kenazi, akafa.”

 

-          Tunasoma tena namna na jinsi Israel walivyofanya uovu na kutoa nafasi ya kuonewa tena walionewa sana na wamidiani na amaleki, walikuwa hata wakilima wakati wa mavuno chakula kilichukuliwa, mifugo ilichukuliwa hawakuwa na amani kiasi cha kuamua kuishi kwenye mashimo kwa ujumla walifanyiwa mambo mabaya neno la Mungu linasema walitwezwa sana ! yaani walionewa mno au walionewa kupita kiasi

 

Waamuzi 6:1-6 “Kisha wana wa Israeli walifanya yaliyo maovu mbele za macho ya Bwana; Bwana akawatia mikononi mwa Midiani muda wa miaka saba Mkono wa Midiani ulikuwa na nguvu juu ya Israeli; tena kwa sababu ya Midiani wana wa Israeli walijifanyia hayo mashimo yaliyo milimani, na hayo mapango, na hizo ngome. Basi ikawa, hapo Israeli walipokuwa wamepanda mashamba, Wamidiani wakakwea, na Waamaleki, na hao wana wa mashariki; wakakwea juu yao; wakapanga marago juu yao, na kuyaharibu hayo maongeo ya nchi, hata ufikapo Gaza, wala hawakuacha katika Israeli riziki ziwazo zote; kondoo, wala ng'ombe, wala punda. Kwa maana walikwea na ng'ombe zao na hema zao, wakaja mfano wa nzige kwa wingi; wao na ngamia zao pia walikuwa hawana hesabu; nao waliingia katika hiyo nchi ili kuiharibu. Israeli walitwezwa sana kwa sababu ya Wamidiani; nao wana wa Israeli wakamlilia Bwana.”

 

Wamidiani walifanya uonevu juu ya wana wa Israel kiasi cha kusikitisha sana mpaka wana wa Israel walipomlilia Bwana ndipo Bwana alimpomuinua Gideoni na maandiko yanaeleza ya kuwa Gideoni alijiliwa na Roho wa Bwana juu yake ambaye alimsaidia kupanga vita na kuleta ushindi kwa askari wachache.

 

Waamuzi 6:33-34 “Wakati huo Wamidiani na Waamaleki, na hao wana wa mashariki walikutana pamoja; wakavuka na kupanga hema zao katika bonde la Yezreeli. Lakini roho ya Bwana ikaja juu yake Gideoni; naye akapiga tarumbeta; na Abiezeri walikutanika na kumfuata.”

 

-          Wana wa Amoni waliwasumbua sana Israel waliwapiga na kuwatawala kiasi ambacho wazee wa mji waliamua kwenda kumuomba Yeftha ili aje awasaidie dhidi ya uonevu na taabu waliyokumbana nayo wakati huo kutoka kwa wana wa Amoni angalia

 

Waamuzi 11:5-7 “Ikatukia, hapo wana wa Amoni walipopigana na Israeli, wazee wa Gileadi wakaenda kumtwaa huyo Yeftha katika ile nchi ya Tobu; wakamwambia Yeftha, Njoo wewe uwe kichwa chetu, ili tupate kupigana na wana wa Amoni. Yeftha akawaambia wazee wa Gileadi, Je! Ninyi hamkunichukia mimi na kunifukuza nitoke katika nyumba ya baba yangu? Basi kwani kunijilia hivi sasa wakati mlio katika taabu?

 

Yeftha aliwezaje kupambana na wana wa Amoni? Maandiko yanaeleza ya kuwa Roho wa Bwana alikuja juu yake na ni Mungu aliyemwenzesha Yeftha, kushindana na mfalme wa wana wa Amani na kuwashinda

 

Waamuzi 11:29-33 “Ndipo roho ya Bwana ikamjilia juu yake Yeftha, naye akapita katika Gileadi na Manase, akapita na katika Mispa ya Gileadi, na kutoka hapo Mispa ya Gileadi akapita kuwaendea wana wa Amoni.Naye Yeftha akamwekea Bwana nadhiri, akasema, Kwamba wewe utawatia wana wa Amoni mkononi mwangu kweli, ndipo itakuwa ya kwamba, kile kitakachotoka katika milango ya nyumba yangu kunilaki, hapo nitakaporudi na amani kutoka kwa hao wana wa Amoni, kitu hicho kitakuwa ni cha Bwana, nami nitakisongeza kiwe sadaka ya kuteketezwa. Basi Yeftha akavuka kuwaendea wana wa Amoni ili kupigana nao; naye Bwana akawaua mkononi mwake. Akawapiga kutoka Aroeri hata kufikilia Minithi, miji ishirini, na mpaka Abel-keramimu, akawapiga kwa machinjo makuu mno. Basi hivyo wana wa Amoni walishindwa mbele ya wana wa Israeli.”

 

-          Wafilisti wakati wote wa maisha ya Samsoni walikuwa waonevu dhidi ya Israel, lakini Mungu alimuinua Samsoni kama mwamuzi ili kuwakomesha wafilisti ni namna gani uonevu huo ulikomesha ilikuwa kupitia Roho Mtakatifu ambaye alimshughulisha Samsoni kwa nguvu angalia;-

 

Waamuzi 15:14-16 “Alipofika Lehi, Wafilisti wakapiga kelele walipokutana naye; ndipo roho ya Bwana ikamjia kwa nguvu, na zile kamba zilizokuwa juu ya mikono yake zikawa kama kitani iliyoteketezwa kwa moto, na vile vifungo vyake vikaanguka mikononi mwake. Naye akaona mfupa mbichi wa taya ya punda, akautwaa, akapiga watu elfu kwa mfupa huo; Samsoni akasema, Kwa taya ya punda chungu juu ya chungu, Kwa taya ya punda nimepiga watu elfu.”

Hitimisho:

Katika vifungu vyote hapo juu somo kubwa tunalojifunza ni kuwa hakuna mahali unaweza kutatua changamoto za uonevu wa aina yoyote ile bila Roho wa Bwana, Katika juma hili la Pentekoste wengi wa wahubiri watafundisha na kukazia kuhusu ujazo wa Roho Mtakatifu, watafundisha umuhimu wa nguvu za Roho Mtakatifu, wataombea watu wajazwe Roho Mtakatifu, watafundisha umuhimu wa kunena kwa Lugha, watafundisha kuhusu ubatizo wa Roho Mtakatifu, watafundisha kunena kwa lugha kama ishara ya ujazo wa roho Mtakatifu, watafundisha mpaka karama za Roho, Watafundisha namna na jinsi Roho wa Mungu anavyosaidia katika kuomba, kutia nguvu, kutupa ujasiri na kadhalika na kadhalika hayo yote ni sawa na ni ya muhimu lakini Roho Mtakatifu ni kwaajili ya nini, ni kwaajili ya kukomesha uonevu, Roho Mtakatifu alipokuwa juu ya masihi Yaani Bwana Yesu tunaona wakati wote alishughulika na walioonewa,  Hata wafalme walipotawala Mungu aliwapaka mafuta ili wakomeshe uonevu dhidi ya watu wake, kanisa katika wakati huu halina budi kurudi kwenye msingi huu, tunamuhitaji Roho Mtakatifu na nguvu zake ili tuwasaidie ndugu zetu kwa kuwatoa katika uonevu wa aina mbalimbali, uonevu wa dhambi, uonevu wa ibilisi, uonevu wa magonjwa, na ana nyingine zote za uonevu!

 Luka 4:18-19 “Roho wa Bwana yu juu yangu, Kwa maana amenitia mafuta kuwahubiri maskini habari njema. Amenituma kuwatangazia wafungwa kufunguliwa kwao, Na vipofu kupata kuona tena, Kuwaacha huru waliosetwa, Na kutangaza mwaka wa Bwana uliokubaliwa.”

Matendo 10:38 “habari za Yesu wa Nazareti, jinsi Mungu alivyomtia mafuta kwa Roho Mtakatifu na nguvu naye akazunguka huko na huko, akitenda kazi njema na kuponya wote walioonewa na Ibilisi; kwa maana Mungu alikuwa pamoja naye

Kwa hiyo Roho Mtakatifu na nguvu zake ni kwaajili ya kuwaokoa wote walioonewa na ibilisi, ni nguvu kwaajili ya kufungua watu, ni nguvu za kuwapa watu ufahamu, kuwafanya vipofu kuona, ni nguvu za kuwaacha huru waliotekwa, na waliosetwa yaani waliogandamizwa na nguvu za giza,  ni nguvu za kuutanganza mwaka wa Bwana uliokubaliwa yaani ni wakati wa kuwaweka huru watu kutoka katika vifungo mbalimbali, Mungu wetu kupitia Roho wake Mtakatifu ataachlia karama na vipawa vikubwa na kuwezesha watu kufanya kazi yake kwa uhodari na kwa hekima na maarifa  na kwa kutenda kazi iliyo njema ya kuwasaidia walioonewa

Na. Rev. Innocent Mkombozi Kamote

Mkuu wa wajenzi mwenye hekima!