Jumapili, 13 Septemba 2026

Waraka huu ukiisha kusomwa kwenu!

 


Wakolosai 4:15-18 “Wasalimuni ndugu walioko Laodikia, na Nimfa, na kanisa lililo katika nyumba yake. Waraka huu ukiisha kusomwa kwenu fanyeni kwamba usomwe katika kanisa la Walaodikia pia; na ule wa Laodikia usomwe na ninyi. Mwambieni Arkipo, iangalie sana huduma ile uliyopewa katika Bwana, ili uitimize. Salamu yangu mimi Paulo, kwa mkono wangu mwenyewe. Kumbukeni kufungwa kwangu. Neema na iwe pamoja nanyi.”



Utangulizi:

Ni muhimu kufahamu kuwa katika nyakati hizi tulizo nazo taarifa husambaa kwa haraka sana kwa njia ya simu, mitandao ya kijamii, televisheni, redio, magazeti na kadhalika, Lakini nyakati za kanisa la Kwanza taarifa zilikuwa zinasambaa kwa kupitia nyaraka tena katika mazingira magumu sana, Paulo mtume aliyekuwa Gerezani alikuwa anataka nyaraka zake anazoziandikia kanisa zisambae kutoka katika kanisa moja na kwenda kanisa lingine kama njia ya kufikisha ujumbe wa injili na mafundisho ya Bwana, Kwa hivyo barua zilikuwa zikizunguka kutoka kanisa moja kwenda kanisa lingine, Paulo hakutaka Neno la Mungu libaki katika kanisa moja tu, badala yake alitaka ziyafikie makanisa yote, Na huu ni ujumbe muhimu sana kwa kanisa la Mungu katika nyakati zetu,Neno la Mungu halipaswi kuwa hatimiliki ya kanisa moja tu na badala yake ujumbe wa neno la Mungu unapaswa kuwafikia watu wote Ona :-

Wakolosai 4:15-18 “Wasalimuni ndugu walioko Laodikia, na Nimfa, na kanisa lililo katika nyumba yake. Waraka huu ukiisha kusomwa kwenu fanyeni kwamba usomwe katika kanisa la Walaodikia pia; na ule wa Laodikia usomwe na ninyi. Mwambieni Arkipo, Iangalie sana huduma ile uliyopewa katika Bwana, ili uitimize. Salamu yangu mimi Paulo, kwa mkono wangu mwenyewe. Kumbukeni kufungwa kwangu. Neema na iwe pamoja nanyi.”

Katika kifungu hiki cha msingi cha neno la Mungu ambacho tunajifunza leo, tunasoma maelekezo ya Paulo Mtume kwa kanisa la Kolosai kwamba waraka wao wahakikishe unasomwa katika kanisa la Laodikia na ule wa Laodikia usomwe na wao, hii inatufundisha somo muhimu sana ya kuwa Neno au ujumbe wa neno la Mungu unaotumiwa na Kanisa moja au aliopewa mtumishi wa Mungu kwaajili ya Kanisa fulani, unaweza pia kutumiwa na Kanisa lingine  kwa makusudi ya kujengana, kutiana moyo, kuhudumia mwili wa Kristo na  kwaajili ya shughuli za kimaongozi, kwa kufanya hivi kanisa litakuwa na umoja na litahitimu katika nia moja.

Waraka wa Kolosai unaweza kusomwa na Laodikia na ule wa Laodikia unaweza kusomwa Kolosai, hii inatufundisha wazi kuwa nyakati za kanisa la kwanza nyaraka za Paulo Mtume na huenda hata na za mitume wengine zilisomwa vilevile katika makanisa mengine na hivyo ufunuo wa hekima wa neno la Mungu  na miongozo mbalimbali ingeweza kuwa na faida na kusaidia kanisa lingine. Na sio hivyo tu mafundisho ya mitume yangelisaidia Kanisa ulimwenguni kote kujenga umoja wa kikanisa na ushirikiano, hii haitofautiani hata kidogo na swala la Paulo mtume kumuagiza Timotheo kuhubiri kile alichokisikia kwake na kuwakabidhi watu waaminifu watakaofaa kuwafundisha wengine:-

2Timotheo 2:2 “Na mambo yale uliyoyasikia kwangu mbele ya mashahidi wengi, hayo uwakabidhi watu waaminifu watakaofaa kuwafundisha na wengine.”

Kwa msingi huo tunajifunza hapa kwamba waraka yaani ujumbe wa Mungu wa kanisa “A” unaweza pia kusomwa “Kuhubiriwa” na Kanisa “B” na ule wa Kanisa “B” ukasomwa  “Kuhubiriwa” na Kanisa “A”, Mungu anapomtumia mtumishi wake kuleta ujumbe kwa Kanisa lake la mahali pamoja, ujumbe huo, huweza kuwafaa watu wa Kanisa lingine, hiki ndicho tunachojifunza kutokana na maelekezo ya Paulo mtume, Jambo kubwa la msingi ni mtumishi wa Mungu kukaa katika hali ya maombi na kuutafasiri ujumbe anaojifunza kutoka kwa wengine katika mazingira ya watu wa Kanisa lake, kwa utulivu huku ukimpa nafasi Roho Mtakatifu kwa sababu yeye ndiye Mwalimu wetu Mkuu.

Na jambo hili linafaa zaidi kama Kanisa au watu wa mahali hapo wanapitia changamoto zinazofanana kama ilivyokuwa kwa Kolosai na Laodikia, aidha inaweza kuwa vema kufanya hivyo kwa sababu sio kila mtu anaweza kuwa mpishi hata kama wote ni familia moja na tunakaa katika nyumba moja, Mungu amewapa neema wengine kuwa na uwezo wa kuandaa jumbe kutokana na mazingira ya utulivu waliyo nayo au karama ya ualimu waliyo nayo na mwingine anaruhusiwa kutumia ikiwa ataona vyema kufanya hivyo na kama itampendeza Roho Mtakatifu kwani Roho Mtakatifu ni mmoja pia. Kufanya hivyo sio kufanya wizi wa kitaarifa “Plagiarism” kwani ujumbe wa Mungu sio taarifa bali ni mafundisho kwa kanisa lote. Kwa sababu hiyo Leo tutachukua muda kujifunza na kutafakari ujumbe wa somo hili lenye kichwa “Waraka huu ukiisha kusomwa kwenu!” kwa kuzingatia vipengele vitatu vofuatavyo:-

·         Waraka huu ukiisha kusomwa kwenu!

·         Fanyeni kwamba usomwe katika kanisa lingine.

·         Faida ya kushirikishana ujumbe wa neno la Mungu.

Waraka huu ukiisha kusomwa kwenu!

Ni muhimu kufahamu kuwa katika Barua yake kwa Wakolosai, Paulo mtume anawapa maagizo ya wazi kuhusu kushirikiana waraka wake na Kanisa lingine la Laodikia. Maagizo haya yanatufundisha  na kutuonyesha umuhimu wa kushirikiana ujumbe wa neno la Mungu na makanisa mengine tofauti tofauti, kwani ujumbe huo una umuhimu wa kipekee kwa Kanisa linapokuja swala la kushirikiana na kuhubiri neno la Mungu, Kanisa ni mwili wa Kristo na kwa sababu hiyo uko umuhimu wa kuhudumiana na ndivyo neno la Mungu linavyoagiza.

1Petro 4:10-11 “kila mmoja kwa kadiri alivyoipokea karama, itumieni kwa kuhudumiana; kama mawakili wema wa neema mbalimbali za Mungu. Mtu akisema, na aseme kama mausia ya Mungu; mtu akihudumu, na ahudumu kwa nguvu anazojaliwa na Mungu; ili Mungu atukuzwe katika mambo yote kwa Yesu Kristo. Utukufu na uweza una yeye hata milele na milele. Amina.”

Wakolosai, Walaodikia na Hierapoli yalikuwa ni makanisa yaliyoanzishwa na Epafra katika Asia ndogo, Epafra ni moja ya watumishi wa Mungu anayetajwa katika waraka wa Wakolosai na Filemoni, alikuwa ni muhubiri wa injili aliyekuwa na umuhimu mkubwa sana katika Kanisa la Kolosai na ni wazi kuwa alihusika kulianzisha Kanisa hilo pamoja na mengine yaliyokuwa Asia na alikuwa akiwaombea sana Wakolosai, Walaodikia na Hierapoli, Lakini pia alikuwa ni mtendakazi wa karibu sana wa Paulo mtume na waliwahi kufungwa pamoja naye gerezani kwaajili ya injili. Ona:-

Wakolosai 4:12-13 “Epafra, aliye mtu wa kwenu, mtumwa wa Yesu Kristo, awasalimu, akifanya bidii siku zote kwa ajili yenu katika maombi yake, ili kwamba msimame wakamilifu na kuthibitika sana katika mapenzi yote ya Mungu. Maana namshuhudia kwamba ana juhudi nyingi kwa ajili yenu, na kwa ajili ya hao walioko Laodikia, na kwa ajili ya hao walioko Hierapoli.”

Filemoni 1:23 “Na pamoja na hayo uniwekee tayari mahali pa kukaa; maana nataraji ya kwamba kwa maombi yenu mtajaliwa kunipata. Epafra, aliyefungwa pamoja nami katika Kristo Yesu, akusalimu;”

Paulo Mtume akiwa na Epafra anaandika waraka kwa Wakolosai na huenda aliandika na waraka mwingine kwa kanisa la Laodikia ambao kwa bahati mbaya hauko katika Biblia yetu leo au inawezekana ulipotea lakini anawaagiza Wakolosai kuwa waraka aliowaandikia wakiisha kuusoma wahakikishe unasomwa na watu wa Laodikia na ule wa Laodikia usomwe pia na Wakolosai, kwa nini Paulo anatoa agizo hili?

1.       Paulo alitaka watu washirikiane kweli ya injili  - Alifahamu kuwa ujumbe wake wa injili ulikuwa na umuhimu mkubwa kwa ulimwengu mzima, alikuwa anatambua kuwa Kanisa ni mwili mmoja na kwa vile waraka wake kwa Wakolosai ulikuwa na mafundisho ya msingi kumuhusu Yesu kama kichwa cha Kanisa na kweli kuhusu wokovu alitamani waraka huo huo ufike Laodikia ili kwamba mafundisho yake yaweze kuwafikiwa wakristo wengi Duniani na wote wajengwe kuwa na imani moja, Paulo alifahamu kuwa neno la Mungu lina pumzi ya Mungu na kwa sababu hiyo linafaa kwa mafundisho sio ya kanisa fulani tu  kla mahali pamoja bali na makanisa mengine:-

 

2Timotheo 3:14-17 “Bali wewe ukae katika mambo yale uliyofundishwa na kuhakikishwa, kwa maana unajua ni akina nani ambao ulijifunza kwao; na ya kuwa tangu utoto umeyajua maandiko matakatifu, ambayo yaweza kukuhekimisha hata upate wokovu kwa imani iliyo katika Kristo Yesu. Kila andiko, lenye pumzi ya Mungu, lafaa kwa mafundisho, na kwa kuwaonya watu makosa yao, na kwa kuwaongoza, na kwa kuwaadibisha katika haki; ili mtu wa Mungu awe kamili, amekamilishwa apate kutenda kila tendo jema.”

 

2.       Paulo mtume alitaka makanisa yote yakabiliane na mafundisho ya uongo – Makanisa yote ya Kolosai na Laodikia yalikuwa yakikabiliwa na changamoto ya mafundisho ya uongo yakiwemo yale ya Kiyahudi yanayochanganya kweli ya injili na sheria za kiyahudi (Jewish legalism) na mafundisho ya “Gnosticism” waliokazia kuwa dhambi ni ujinga na wokovu unaletwa na ufahamu au maarifa, aidha pia watu walikuwa wakifundisha maono na ndoto ambazo kimsingi hazikuwa kweli ya neno la Mungu,Walifundisha kushika sabato, kuandama mwezi na baadhi ya maswala ya sheria tofauti na kweli ya injili, Yalikuweko pia mafundisho yahusuyo kuutesa mwili, msishike, msiguse wala msionje (Asceticism) Paulo alitaka makanisa yote yapokee mafundisho safi na ya kweli yanayomzingatia Kristo, sio hivyo tu Mitume walitaka mafundisho yao yaenezwe katika makanisa yote na watu wayashike, na kama mtu haleti mafundisho hayo waliagiza asikaribishwe, wala wasitamani kula naye maana kufanya hivyo ni kuunga mkono mafundisho potofu. Adui wa Kolosai alikuwa ndiye adui wa Laodikia kwa hiyo kwa kushirikiana nyaraka za kitume makanisa yote yangeimarika kwa fundisho sahihi.

 

Wakolosai 2:16-19 “Basi, mtu asiwahukumu ninyi katika vyakula au vinywaji, au kwa sababu ya sikukuu au mwandamo wa mwezi, au sabato; mambo hayo ni kivuli cha mambo yajayo; bali mwili ni wa Kristo. Mtu asiwanyang'anye thawabu yenu, kwa kunyenyekea kwa mapenzi yake mwenyewe tu, na kuabudu malaika, akijitia katika maono yake na kujivuna bure, kwa akili zake za kimwili; wala hakishiki Kichwa, ambacho kwa yeye mwili wote ukiruzukiwa na kuungamanishwa kwa viungo na mishipa, hukua kwa maongeo yatokayo kwa Mungu.”      

 

2Yohana 1:7-10 “Kwa maana wadanganyifu wengi wametokea duniani, wasiokiri ya kuwa Yesu Kristo yuaja katika mwili. Huyo ndiye yule mdanganyifu na mpinga Kristo. Jiangalieni nafsi zenu msiyapoteze mliyoyatenda, bali mpokee thawabu timilifu.Kila apitaye cheo, wala asidumu katika mafundisho ya Kristo, yeye hana Mungu. Yeye adumuye katika mafundisho hayo, huyo ana Baba na Mwana pia. Mtu akija kwenu, naye haleti mafundisho hayo, msimkaribishe nyumbani mwenu, wala msimpe salamu.”

 

3.       Paulo alitaka kanisa linie mamoja Kanisa ni mwili mmoja – Ingawa Kanisa la Kolosai na Laodikia yalikuwa katika sehemu tofauti au miji mbalimbali tofauti kushirikiana kwao nyaraka au mafundisho ya mtume kulimaanisha kuwa Kanisa ni mwili mmoja, Paulo alilenga kuyafanya makanisa haya kuwa ndugu na kutaka kuimarisha uhusiano katika ya kanisa moja na jingine kwa hiyo kushirikiana mafundisho halikuwa jambo baya, Biblia inapoelezea kuwa Kanisa ni mwili mmoja bado pia inaelezea ya kuwa lina viungo vingi, kwa maana hiyo ingawa Kanisa ni moja lakini lina karama na utendaji tofauti tofauti, lakini ingawa mwili ni mmoja  na una viungo vingi hiyo haimaanishi kwamba mwili unaweza kula chakula tofauti tofauti kwaajili ya kila kiungo, chakula ni kimoja, kwa hiyo Kanisa ni moja na utendaji ni tofauti, tunaujenga mwili ule ule!

 

1Wakorintho 12:12-27 “Maana kama vile mwili ni mmoja, nao una viungo vingi, na viungo vyote vya mwili ule, navyo ni vingi, ni mwili mmoja; vivyo hivyo na Kristo.Kwa maana katika Roho mmoja sisi sote tulibatizwa kuwa mwili mmoja, kwamba tu Wayahudi, au kwamba tu Wayunani; ikiwa tu watumwa au ikiwa tu huru; nasi sote tulinyweshwa Roho mmoja.Kwa maana mwili si kiungo kimoja, bali ni vingi. Mguu ukisema, Kwa kuwa mimi si mkono, mimi si wa mwili; je! Si wa mwili kwa sababu hiyo? Na sikio likisema, Kwa kuwa mimi si jicho, mimi si la mwili; je! Si la mwili kwa sababu hiyo? Kama mwili wote ukiwa jicho, ku wapi kusikia? Kama wote ni sikio ku wapi kunusa? Bali Mungu amevitia viungo kila kimoja katika mwili kama alivyotaka. Lakini kama vyote vingekuwa kiungo kimoja, mwili ungekuwa wapi? Lakini sasa viungo ni vingi, ila mwili ni mmoja. Na jicho haliwezi kuuambia mkono, Sina haja na wewe; wala tena kichwa hakiwezi kuiambia miguu, Sina haja na ninyi. Bali zaidi sana vile viungo vya mwili vidhaniwavyo kuwa vinyonge zaidi vyahitajiwa zaidi. Na vile viungo vya mwili vidhaniwavyo kuwa havina heshima, viungo vile twavipa heshima zaidi; na viungo vyetu visivyo na uzuri vina uzuri zaidi sana. Kwa maana viungo vyetu vilivyo na uzuri havina uhitaji; bali Mungu ameuungamanisha mwili, na kukipa heshima zaidi kile kiungo kilichopungukiwa; ili kusiwe na faraka katika mwili, bali viungo vitunzane kila kiungo na mwenziwe. Na kiungo kimoja kikiumia, viungo vyote huumia nacho, na kiungo kimoja kikitukuzwa, viungo vyote hufurahi pamoja nacho. Basi ninyi mmekuwa mwili wa Kristo, na viungo kila kimoja peke yake.”

 

4.       Paulo Mtume alitaka kuweka sawa mtazamo wa kitheolojia kuhusu ubora wa Kristo – Nyaraka yake ilikuwa inabeba mtazamo sahihi wa ubora wa Yesu Kristo na sadaka yake ya upatanisho aliyoitoa msalabani, Paulo anamuelezea Yesu Kristo kwa mtazamo wa juu sana akionyesha kuwa Yeye ni Muumba wa vitu vyote na kuwa katika yeye unakaa utimilifu wote wa Mungu na kwa sababu hiyo alitaka ujumbe huu ueleweke wazi kwa makanisa yote ambayo kimsingi yalikuwa yanashirikiana eneo moja la kijiografia na hivyo ilikuwa ni wazi kuwa mafundisho yanayoshusha heshima ya Kristo yangeweza kuyaathiri makanisa yote mawili na zaidi hivyo kubadilishana nyaraka kungelifanya wawe na msimamo mmoja  na kauli moja na uhakika kutoka kwa mtume

 

Wakolosai 1:15-20 “naye ni mfano wa Mungu asiyeonekana, mzaliwa wa kwanza wa viumbe vyote. Kwa kuwa katika yeye vitu vyote viliumbwa, vilivyo mbinguni na vilivyo juu ya nchi, vinavyoonekana na visivyoonekana; ikiwa ni vitu vya enzi, au usultani, au enzi, au mamlaka; vitu vyote viliumbwa kwa njia yake, na kwa ajili yake. Naye amekuwako kabla ya vitu vyote, na vitu vyote hushikana katika yeye. Naye ndiye kichwa cha mwili, yaani, cha kanisa; naye ni mwanzo, ni mzaliwa wa kwanza katika wafu, ili kwamba awe mtangulizi katika yote. Kwa kuwa katika yeye ilipendeza utimilifu wote ukae; na kwa yeye kuvipatanisha vitu vyote na nafsi yake akiisha kufanya amani kwa damu ya msalaba wake; kwa yeye, ikiwa ni vitu vilivyo juu ya nchi, au vilivyo mbinguni.”

 

Wakolosai 2:13-15 “Na ninyi mlipokuwa mmekufa kwa sababu ya makosa yenu na kutokutahiriwa kwa mwili wenu, aliwafanya hai pamoja naye, akiisha kutusamehe makosa yote; akiisha kuifuta ile hati iliyoandikwa ya kutushitaki kwa hukumu zake, iliyokuwa na uadui kwetu; akaiondoa isiwepo tena, akaigongomea msalabani; akiisha kuzivua enzi na mamlaka, na kuzifanya kuwa mkogo kwa ujasiri, akizishangilia katika msalaba huo.               

 

5.       Paulo alikuwa na ufahamu kuwa ujumbe anaouandika haukuwa kwaajili ya kanisa la mahali pamoja tu, ulikuwa pia kwaajili ya sehemu nyingine, Hakuna kanisa ambalo linaweza kudai kuwa fundisho walilonalo ni la kwao peke yao, wala muhubiri mmoja kudhani kuwa ujumbe anaopewa na Roho Mtakatifu ni wa kwake tu, Nataka nikuhakikishie kuna wachoyo wengi sana wana jumbe hawaandiki, wala hawazirushi katika mitandao ya kijamii kwa sababu wanadhani ni za kwao tu na za kanisa lake la mahali pamoja au wanataka kuzifanyia biashara “you cant monopolize the Gospel as if it belongs  you alone” “huwezi kuhodhi injili kana kwamba ni mali yako pekee” Mungu hajakuita kwaajili ya kanisa la mahali pamoja tu sidhani kama uko wito wa namna hiyo Mungu ametuita kwaajili ya mataifa yote, unaporejea kwenye kanisa lako la mahali pamoja umerudi tu kwenye nyumba yako, au kituo chako cha nyumbani lakini linapokluja swala la injili sio ya mahali pamoja ni ya dunia nzima. Pailo mtume alikuwa anafahamu asili ya witio wake kuwa jni wito kwa mataifa yote, na agizo kuu pia limeagiza kwamba injili ihubiriwe ulimwenguni kote enendendi ulimwenguni kote!

 

Matendo 9:15-16. “Lakini Bwana akamwambia, Nenda tu; kwa maana huyu ni chombo kiteule kwangu, alichukue Jina langu mbele ya Mataifa, na wafalme, na wana wa Israeli. Maana nitamwonyesha yalivyo mengi yatakayompasa kuteswa kwa ajili ya Jina langu.”

 

Warumi 11:13 “Lakini nasema na ninyi, mlio watu wa Mataifa. Basi, kwa kadiri nilivyo mtume wa watu wa Mataifa, naitukuza huduma iliyo yangu, nipate kuwatia wivu walio damu moja na mimi na kuwaokoa baadhi yao.”

 

Wagalatia 1:15-16 “Lakini Mungu, aliyenitenga tangu tumboni mwa mama yangu, akaniita kwa neema yake, alipoona vema kumdhihirisha Mwanawe ndani yangu, ili niwahubiri Mataifa habari zake; mara sikufanya shauri na watu wenye mwili na damu;”     

 

Mwanzo 12:1-3 “BWANA akamwambia Abramu, Toka wewe katika nchi yako, na jamaa zako, na nyumba ya baba yako, uende mpaka nchi nitakayokuonyesha; nami nitakufanya wewe kuwa taifa kubwa, na kukubariki, na kulikuza jina lako; nawe uwe baraka;nami nitawabariki wakubarikio, naye akulaaniye nitamlaani; na katika wewe jamaa zote za dunia watabarikiwa.”

 

Unaona Mungu anapomuita mtumishi wake hamuiti kwaajili ya kanisa la mahali pamoja tu, kujidhania kuwa umeitwa kwaajili ya sehemu moja tu ni kosa la kiufundi, wewe ni sauti ya Mungu kutoka pale ulipo kuelekea kila mahali ulimwenguni, Mungu aliponiita mimi katika huduma hii, aliniambia nitakufanya kuwa fundi mkuu utatengeneza matofali, kisha utawapa watu wataijenga nyumba yangu kila mahali ulimwenguni, ndio maana ya mkuu wa wajenzi, tunaujenga mwili wa Kristo, mtu akitumia jumbe zangu nafurahi sana kwa sababu kile ambacho Mungu amenipa kinaenea duniani kote, na haya ndio mapenzi ya Mungu, na tangu nimeanza kufanya hivyo sijawahi kupungukiwa na jumbe, Roho Mtakatifu amekuwa mwaminifu akinipa Jumbe kila wakati kwaajili yenu,  kwaajili ya mwili wa Kristo, zitumieni kama Bwana anavyowaongoza, sijisikii vibaya watu wakihudumu na kuhubiri jumbe zangu kwa sababu zimekuwa Baraka kubwa kila mahali ulimwenguni, zinawafikia watu Msumbiji, Kongo, Kenya, Rwanda, Burundi, Marekani, Tanzania na maeneo mbalimbali na hii ni furaha yangu! Na kama wewe unavyobarikiwa na kushangaa, na mimi baada ya kumaliza kuandaa, huwa nabarikiwa na ninashangaa, kwamba hivi mimi nawezaje kuwa natengeneza jumbe kali namna hii sio mimi ni Roho wa Mungu! Utukufu ni wake!

Fanyeni kwamba usomwe katika kanisa lingine.

Kimsingi neno la Mungu linaonyesha kuwa sio dhambi kwa watumishi wa Mungu kushirikishana mafundisho, Neno la Mungu linaonyesha kuwa mafundisho yanapokelewa, yanahifadhiwa, na yanapitishwa kutoka kizazi kimoja hata kizazi kingine na kwa sababu hiyo tunajifunza kwamba sio dhambi kufundisha kile ulichofundishwa na ukawafundisha watu wengine!

2Timotheo 2:2 “Na mambo yale uliyoyasikia kwangu mbele ya mashahidi wengi, hayo uwakabidhi watu waaminifu watakaofaa kuwafundisha na wengine.”

Kila mtumishi wa Mungu ana wajibika kutunza maudhui sahihi ya mafundisho au maneno aliyoyasikia au kuyasoma kutoka kwa wale waliojaliwa kuandika neno la Mungu, kufundisha kwa usahihi na kwa uaminifu  kile ulichojifunza kutoka kwa wale unaowaamini au wale wenye imani moja na wewe, Mungu anachokitaka ni ile kweli ilindwe, wakati huo huo tusiache kusoma na kuchimba maandiko na kujiachia mbele za Roho Mtakatifu ili tuweze kupokea ufunuo sahihi unaoendana sawa na neno la Mungu, tunatofautiana neema, mtazamo na uzoefu na karama au vipawa kwa hiyo kila mmoja atafanya kwa kadiri ya neema aliyopewa, Kabla ya kuandika injili yake Luka alikuwa amesoma injili zilizotangulia kuandikwa na nyingine, kama injili ya Marko na Mathayo, hivyo yeye naye aliamua kuandika kwa jinsi yake japokuwa injili zote zina lengo lile lile la kuelezea maisha na mafundisho ya Bwana, Marko, Mathayo na Luka zinaitwa injili zinazofanana. “Synoptic Gospel” Lakini zikiwa na lengo moja, hata hivyo Luka anaandika katika namna inayovutia zaidi na alifanya hivyo baada ya kufanya utafiti wa kutosha ona:-

Luka 1:1-4 “Kwa kuwa watu wengi wametia mikono kutunga kwa taratibu habari za mambo yale yaliyotimizwa katikati yetu, kama walivyotuhadithia wale waliokuwa mashahidi wenye kuyaona, na watumishi wa lile neno tokea mwanzo, nimeona vema mimi nami, kwa kuwa nimejitafutia usahihi wa mambo hayo yote tangu mwanzo, kukuandikia kwa taratibu, Theofilo mtukufu,upate kujua hakika ya mambo yale uliyofundishwa.”

Unaona Mathayo, Marko, Luka na hata Yohana wote wanaandika habari za Yesu Kristo mafundisho yake na matendo yake lakini kila mmoja akiwa na kionjo tofauti kwa aina yake,  basi tuupeleke ujumbe wa injili kwa watu wote kwa kadiri ya neema ya Mungu kila mtu kwa kionjo chake lakini lengo likiwa moja kujenga mwili wa Yesu yaani kanisa.

Paulo anachoagiza sasa anataka makanisa yote yashirikiane neno la Mungu, Mungu anaweza kuzungumza na Kanisa lake kupitia ujumbe mmoja, Kanisa la Kolosai na Laodikia walipaswa kushirikiana neno la Mungu lakini pia walifanya hivyo kwa makanisa mengine, ushirikiano wa neno la Mungu ulipunguza gharama, ulisaidia kuwa na sauti ya umoja, kujilinda na mafundisho ya uongo, Kanisa kuwa na fundisho lililo sahihi kwa pamoja, kwa hiyo Kanisa la Kolosai linapokea Waraka wa Paulo na kanisa la Laodikia linapokea waraka wa Paulo, Kisha Laodikia wanawashirikisha Kolosai na Kolosai wanawashirikisha Laodikia, wote wanapata kopi na wote wanakuwa salama, huu ndio mpango na makusudi ya Mungu. 

Wakolosai 4:15-18 “Wasalimuni ndugu walioko Laodikia, na Nimfa, na kanisa lililo katika nyumba yake. Waraka huu ukiisha kusomwa kwenu fanyeni kwamba usomwe katika kanisa la Walaodikia pia; na ule wa Laodikia usomwe na ninyi. Mwambieni Arkipo, iangalie sana huduma ile uliyopewa katika Bwana, ili uitimize. Salamu yangu mimi Paulo, kwa mkono wangu mwenyewe. Kumbukeni kufungwa kwangu. Neema na iwe pamoja nanyi.”

Faida ya kushirikishana ujumbe wa neno la Mungu.

Wakristo wanaposhirikiana neno la Mungu kuna faida kadhaa zinajitokeza katika mwili wa Kristo zinaweza kuwepo faida nyingi sana lakini kikubwa wote tunahitimu katika nia moja na kunena mamoja, kukuza imani yetu pamoja, kukua kiroho pamoja, kujilinda katika imani kwa pamoja na kutokutofautiana kwa kiwango kikubwa kati ya Kanisa moja na lingine, kimisimamo na kimafundisho.

1Wakorintho 1:10-13. “Basi ndugu, nawasihi, kwa jina la Bwana wetu Yesu Kristo, kwamba nyote mnene mamoja; wala pasiwe kwenu faraka, bali mhitimu katika nia moja na shauri moja. Kwa maana, ndugu zangu, nimearifiwa habari zenu na wale walio wa nyumbani mwa Kloe, ya kwamba iko fitina kwenu. Basi, maana yangu ni hii, ya kwamba kila mtu wa kwenu kusema, Mimi ni wa Paulo, na, Mimi ni wa Apolo, na, Mimi ni wa Kefa, na, Mimi ni wa Kristo. Je! Kristo amegawanyika? Je! Paulo alisulibiwa kwa ajili yenu? Au je! Mlibatizwa kwa jina la Paulo?

1Petro 2:2-5 “Kama watoto wachanga waliozaliwa sasa yatamanini maziwa ya akili yasiyoghoshiwa, ili kwa hayo mpate kuukulia wokovu; ikiwa mmeonja ya kwamba Bwana ni mwenye fadhili. Mmwendee yeye, jiwe lililo hai, lililokataliwa na wanadamu, bali kwa Mungu ni teule, lenye heshima. Ninyi nanyi, kama mawe yaliyo hai, mmejengwa mwe nyumba ya Roho, ukuhani mtakatifu, mtoe dhabihu za roho, zinazokubaliwa na Mungu, kwa njia ya Yesu Kristo.”

Wakolosai 1:26-28 “siri ile iliyofichwa tangu zamani zote na tangu vizazi vyote, bali sasa imefunuliwa kwa watakatifu wake; ambao Mungu alipenda kuwajulisha jinsi ulivyo utajiri wa utukufu wa siri hii katika Mataifa, nao ni Kristo ndani yenu, tumaini la utukufu ambaye sisi tunamhubiri habari zake tukimwonya kila mtu, na kumfundisha kila mtu katika hekima yote, tupate kumleta kila mtu mtimilifu katika Kristo”.

Ukiacha kuhitimu katika nia moja, kuukulia wokovu kwa viwango vinavyoendana, kuwa watumilifu kama Kristo, vile vile Kanisa tunaweza kujihami na mafundisho ya uongo yanayoingia kwa kasi hususani katika nyakati hizi za mwisho, Kanisa la Kolosai liliingiliwa na mafundisho ya uongo ambayo kama wao walitahadharishwa ingelikuwa rahisi kwa Kanisa la Laodikia pia kuchukua tahadhari mapema kabla hayajawakuta.

Wakolosai 2:6-8 “Basi kama mlivyompokea Kristo Yesu, Bwana, enendeni vivyo hivyo katika yeye; wenye shina na wenye kujengwa katika yeye; mmefanywa imara kwa imani, kama mlivyofundishwa; mkizidi kutoa shukrani. Angalieni mtu asiwafanye mateka kwa elimu yake ya bure na madanganyo matupu, kwa jinsi ya mapokeo ya wanadamu, kwa jinsi ya mafundisho ya awali ya ulimwengu, wala si kwa jinsi ya Kristo. Maana katika yeye unakaa utimilifu wote wa Mungu, kwa jinsi ya kimwili.”

Unaona kwa tahadhari kama hii basi uongo unadhibitiwa mapema, wakristo wanaweza kushauriana na kutiana moyo, na umoja wa makanisa unaimarika na mwili wa Kristo unajengwa

Inarahisisha kuenea kwa injili, Paulo mtume alikuwa kizuizini, alikuwa amefungwa lakini neno la Mungu halifungwi, Paulo angeliweza kama mtume kuufikisha ujumbe katika makanisa hata bila yaye ye kufika  na injili ingeenea na ingeenea kwa usahihi, injili inawafikia watu wengi zaidi, kila Kanisa linafanyika kituo cha injili, Kanisa linaimarika, makanisa yanazaliwa, imani inajengwa, Paulo alitambua ya kuwa ana kitu na kitu hicho kinatakiwa kuwafikia watu wengi, akiwa amefungwa angewezaje kuufikisha ujumbe ni kwa kuandika, kuishirikisha injili kila mahali ni agizo la Kristo

Marko 16:15-16 “Akawaambia, Enendeni ulimwenguni mwote, mkaihubiri Injili kwa kila kiumbe. Aaminiye na kubatizwa ataokoka; asiyeamini, atahukumiwa.”

1Petro 3:15 “Mwe tayari siku zote kumjibu kila mtu awaulizaye habari za tumaini lililo ndani yenu; lakini kwa upole na kwa hofu.”

Warumi 1:1-6 “Paulo, mtumwa wa Kristo Yesu, aliyeitwa kuwa mtume, na kutengwa aihubiri Injili ya Mungu;ambayo Mungu amekwisha kuiahidi kwa kinywa cha manabii wake katika maandiko matakatifu; yaani, habari za Mwanawe, aliyezaliwa katika ukoo wa Daudi kwa jinsi ya mwili,na kudhihirishwa kwa uweza kuwa Mwana wa Mungu, kwa jinsi ya roho ya utakatifu, kwa ufufuo wa wafu, Yesu Kristo Bwana wetu; ambaye katika yeye tulipokea neema na utume ili mataifa yote wapate kujitiisha kwa imani, kwa ajili ya jina lake; ambao katika hao ninyi mmekuwa wateule wa Yesu Kristo;”

Hitimisho:

Kwa hiyo tunajifunza ya kuwa nyakati za Kanisa la Kwanza mitume walishirikisha watu wote neno la Mungu na mafundisho yao, baadae nyaraka hizo zilikuswanywa pamoja na kufanyika neno la Mungu yaani Biblia tuliyo nayo, hata hivyo Biblia inahitaji utaalamu kuitafasiri na sio watu wote wanaweza lakini wale walioitwa kuwa walimu wanaweza kufanya huduma yao kwa bidii na kuwasaidia wakristo kuifahamu kweli ya neno la Mungu kwa jumbe zao, kwa hiyo ni vema ujumbe huu ukawafikia makanisa yote endapo utabaini kuwa unaweza kuwasaidia na jumbe nyinginezo zote, waraka huu ukiisha kusomwa kwenu, fanyeni kwamba usomwe katika Kanisa lingine na faida yake utaiona Bwana atupe neema, kumfundisha kila mtu neno la Mungu ili injili iweze kuwafikia watu wote kwa utukufu wa Mungu Baba mwenyewe

Warumi 12:4-8 “Kwa kuwa kama vile katika mwili mmoja tuna viungo vingi, wala viungo vyote havitendi kazi moja; Vivyo hivyo na sisi tulio wengi tu mwili mmoja katika Kristo, na viungo, kila mmoja kwa mwenzake. Basi kwa kuwa tuna karama zilizo mbalimbali, kwa kadiri ya neema mliyopewa; ikiwa unabii, tutoe unabii kwa kadiri ya imani; ikiwa huduma, tuwemo katika huduma yetu; mwenye kufundisha, katika kufundisha kwake; mwenye kuonya, katika kuonya kwake; mwenye kukirimu, kwa moyo mweupe; mwenye kusimamia kwa bidii mwenye kurehemu, kwa furaha.”

Wakolosai 4:16-18. “Waraka huu ukiisha kusomwa kwenu fanyeni kwamba usomwe katika kanisa la Walaodikia pia; na ule wa Laodikia usomwe na ninyi.Mwambieni Arkipo, Iangalie sana huduma ile uliyopewa katika Bwana, ili uitimize. Salamu yangu mimi Paulo, kwa mkono wangu mwenyewe. Kumbukeni kufungwa kwangu. Neema na iwe pamoja nanyi.”                

Na Rev. Innocent Samuel Kamote

Mkuu wa wajenzi mwenye hekima

Jumapili, 6 Septemba 2026

Nafsi yangu imeokoka kama ndege!


Zaburi 124:6-8 “Na ahimidiwe Bwana; Asiyetutoa kuwa mawindo kwa meno yao. Nafsi yetu imeokoka kama ndege Katika mtego wa wawindaji, Mtego umevunjika, nasi tumeokoka. Msaada wetu u katika jina la Bwana, Aliyezifanya mbingu na nchi.”




Utangulizi:

Ni muhimu kufahamu kuwa na hekima na maarifa yatakayokusaidia kujua namna inavyokupasa kuenenda katika ulimwengu huu wenye hila nyingi, ili uweze kujihami na kuwa salama, Katika maisha haya yenye maadui wengi!

Wakati mwingine katika maisha watakuwepo watu wenye hila, ambao kimsingi, watataka kukudhibiti, au kukuwekea mipaka katika maisha, huduma, biashara, masomo na kazi na hata kutaka kukupotezea muda kukutawala na kukukandamiza ili uwatumikie au kile kitu ambacho Mungu amekiweka ndani yako kisiweze kufanya kazi katika mazingira makuu  ya uhuru yaliyokusudiwa na Mungu au ili wewe usitoke kimaisha na ikiwezekana uendelee kuwa mtumwa wa kazi wajibu na fikra za mtawala mjanja ambaye anaweza kukunyima njia ya kujichagulia, kukunyima uhuru wa kujitegemea kuwa na maamuzi yako mwenyewe na kujiendeleza kwa sababu ya hofu yake, wivu wake au mawazo machafu hila na wao ndio wawe na maamuzi juu ya maisha yako siku zote angalia:-

Kutoka 1:8-11 “Basi akainuka mfalme mpya kutawala Misri, asiyemjua Yusufu. Akawaambia watu wake, Angalieni, watu wa wana wa Israeli ni wengi tena wana nguvu kuliko sisi. Haya! Na tuwatendee kwa akili, wasije wakaongezeka; tena, ikitokea vita, wao nao wasije wakashikamana na adui zetu na kupigana nasi, na kutoka katika nchi hii. Basi wakaweka wasimamizi juu yao wawatese kwa mizigo yao. Nao wakamjengea Farao miji ya kuwekea akiba, Pithomu na Ramesesi

Hali kama hii ndio ilikuwa sababu kubwa ya mtawala mpya katika Misri kuwaogopa Israel na kuanza kuweka mitego ya kuwadhoofisha ili ikiwezekana waweze kumezwa na wamisri na kufutika juu ya uso wa Dunia, kama sio mkono wa Mungu ulioonyooshwa na kuwatetea isingelikuwa rahisi Israel kutoka Misri, Hali hii sio stori ya Israel tu ni stori ya kila mtu amwaminiye Mungu duniani katika mikono ya adui yetu mkuu shetani na maajenti wake ambaye ndiye anataka kuitawala nafsi yako!.

Daudi na watu wake wanamshukuru Mungu kwa ukombozi wake na kwa mkono wake ulionyooshwa hata kuwapa Israel ushindi, inaonekana wazi kabisa ujanja wa adui ulikuwa wa kimkakati na wenye ulaghai mwingi sana, adui alikuwa amejipanga kuwatumikisha watu wa Mungu na  kuwabana kiasi ambacho wasingeliweza kupata msaada; mwenyewe anaona mpango wa adui ulikuwa ni kuwameza wakiwa hai, Kumezwa ukiwa hai ni kuchukuliwa mateka na kunyimwa uhuru wako huku ukiteswa nafsi yako  na kutumikishwa  ukiwa umefungwa kabisa kiasi ambacho ni mpaka usaidiwe na mtu wa nje hivi ndivyo adui alivyokuwa amemkusudia Daudi na jamii yake iliyokuwa ikimzunguka. Ona:-

Zaburi 124:1-5 “Kama si Bwana aliyekuwa pamoja nasi, Israeli na aseme sasa, Kama si Bwana aliyekuwa pamoja nasi, Wanadamu walipotushambulia. Papo hapo wangalitumeza hai, Hasira yao ilipowaka juu yetu Papo hapo maji yangalitugharikisha, Mto ungalipita juu ya roho zetu; Papo hapo yangalipita juu ya nafsi zetu Maji yafurikayo

Daudi anaizungumzia hali iliyoikuta nafsi yake na jamii yake sawa na ndege aliyetegewa mtego kisha akakamatika na kuwekwa tunduni, ndege huyu angekosa uhuru wake na maamuzi yake na angetawaliwa maisha yake yangekuwa chini ya amri ya aliyemkamata na kumwekea mtego tu, kama ndege asiyekuwa na nguvu katika mikono ya utawala wa watega mitego isingekuwa rahisi kupata ukombozi mpaka mtu mwenye nguvu zaidi aje akukomboe, Kwa hiyo Daudi na wenzake wanauona wokovu walioupata kuwa sio swala la kubahatisha  bali ni tendo la Mungu mwenye nguvu kuingilia kati na kuivunja mitego ya adui na ndipo nafsi zao zikaokoka na ndio maana katika Zaburi hii anamhimidi Bwana ambaye alizuia kwa namna zote wao kuwa mawindo ya adui na kuwaokoa:-

Wakolosai 1:13-14 “Naye alituokoa katika nguvu za giza, akatuhamisha na kutuingiza katika ufalme wa Mwana wa pendo lake; ambaye katika yeye tuna ukombozi, yaani, msamaha wa dhambi;”

Leo katika mpango wa Mungu tutachukua muda kujifunza somo hili “Nafsi yangu imeokoka kama ndege” kwa kuzingatia vipengele vitatu muhimu vifuatavyo:-

 

·         Ndege katika mtego wa wawindaji.

·         Nafsi katika mitego ya wawindaji.

·         Nafsi yangu imeokoka kama ndege.

 

Ndege katika mtego wa wawindaji.

Zaburi 124:6-8 “Na ahimidiwe Bwana; Asiyetutoa kuwa mawindo kwa meno yao. Nafsi yetu imeokoka kama ndege Katika mtego wa wawindaji, Mtego umevunjika, nasi tumeokoka.  Msaada wetu u katika jina la Bwana, Aliyezifanya mbingu na nchi.”

Ni muhimu kufahamu kuwa kama kuna viumbe wameumbwa wakiwa na uhuru wa asili, basi Ndege ni kiumbe aliyeumbwa akiwa na uhuru huo wa asili, wana uhuru wa asili na mpana sana waliopewa na Mungu, lakini sio hivyo tu ni viumbe ambao Mungu anawajali kiasi kwamba hawana hofu ya maisha, Mungu mwenyewe anawalisha na kuwatunza kwa kiwango cha ajabu sana, Ndege wana ulinzi wa ajabu sana kwa mujibu wa Biblia hakuna ndege anayeanguka bila mbingu kuwa na taarifa, kwa hiyo ndege ni kiumbe chenye ulinzi wa ajabu kutoka kwa Mungu.

Mwanzo 1:20-22 “Mungu akasema, Maji na yajawe kwa wingi na kitu kiendacho chenye uhai, na ndege waruke juu ya nchi katika anga la mbingu. Mungu akaumba nyangumi wakubwa, na kila kiumbe chenye uhai kiendacho, ambavyo maji yalijawa navyo kwa wingi kwa jinsi zao, na kila ndege arukaye, kwa jinsi yake; Mungu akaona ya kuwa ni vyema. Mungu akavibarikia, akisema, Zaeni, mkaongezeke, mkayajaze maji ya baharini, ndege na wazidi katika nchi.”

Mathayo 6:25-26 “Kwa sababu hiyo nawaambieni, Msisumbukie maisha yenu, mle nini au mnywe nini; wala miili yenu, mvae nini. Maisha je! Si zaidi ya chakula, na mwili zaidi ya mavazi? Waangalieni ndege wa angani, ya kwamba hawapandi, wala hawavuni, wala hawakusanyi ghalani; na Baba yenu wa mbinguni huwalisha hao. Ninyi je! Si bora kupita hao?

Mathayo 10:28-31 “Msiwaogope wauuao mwili, wasiweze kuiua na roho; afadhali mwogopeni yule awezaye kuangamiza mwili na roho pia katika jehanum. Je! Mashomoro wawili hawauzwi kwa senti moja? Wala hata mmoja haanguki chini asipojua Baba yenu; lakini ninyi, hata nywele za vichwa vyenu zimehesabiwa zote. Msiogope basi; bora ninyi kuliko mashomoro wengi.”

Unaona Mungu amewaumba ndege wawe na uhuru mpana wa asili, waitamalaki dunia vyovyote wapendavyo, Ndege wanatunzwa na Mungu, hawaangaiki kulima wala kuweka ghalani, lakini Mungu anawalisha, wana furaha wana amani, lakini zaidi ya yote Mungu anawajali kiasi ambacho hawaanguki chini bila mbingu kuwa na taarifa, Lakini changamoto kubwa ya ndege ni wawindaji, Mwanadamu ni kiumbe wa maana zaidi kuliko ndege, Mungu anamjali mwanadamu katika namna isiyoweza kuelezeka Mwandishi mmoja mpka akamuhoji Mungu, Mtu ni kitu gani hata umwangalie

Hata hivyo adui mkubwa wa mwanadamu ni mwanadamu, Mwanadamu ambaye wakati wewe ukiwa huna madhara kwa mtu wala huwazii mabaya juu ya mtu, wawindaji wanakuwazia mabaya na wanataka kuitega nafsi yako, Ndege ni kiumbe dhaifu sana na kuna watu wanataka kumkamata ili wamweke katika tundu, hapo wanataka ndege awe na uhuru finyu, na walimshe wao badala ya Mungu, huu ndio mkakati wa shetani, yeye anataka kuikamata nafsi yako, aifunge akutumikishe usifurahie ule uhuru na maisha uliyopewa na Mungu, leo hata kama nasfi yako imekamatika ninakutangazia kuwa ni siku ya kwenda kuzifungulia nasfi zilizofungwa na kuwekewa mipaka katika jina la Yesu Kristo mwana wa Mungu aliye hai.

Wawindaji sio watu wazuri hata kidogo, wao mpango wao ni kuikamata nafsi yako, na hili ndilo jangwa kubwa sana la kiroho hapa duniani  yaani pale nafsi yako inapokuwa imekamatika, Maandiko yanaonyesha kuwa mtu akifanikiwa kuiteka nafsi yako hususani kama ni adui anaweza kukuweka katika hali ya hatari kubwa sana na kusababisha uharibifu mkubwa wa kiroho na kuitishia usalama wako na kukukosesha amani katika maisha, Waandishi wa Zaburi mara kwa mara wameonyesha kuwa adui anaziwinda nafsi zetu na ili uweze kupata msaada kama umekamatika au unawindwa basi ni Mungu peke yake  ndiye anayeweza kukusaidia na kukuokoa na kuirejesha nafsi yako katika uhuru wake ona:-

Zaburi 7:1-2 “Bwana, Mungu wangu, nimekukimbilia Wewe, Uniokoe na wote wanaonifuatia, uniponye. Asije akaipapura nafsi yangu kama simba, Akiivunja-vunja pasipokuwa na wa kuponya.”

Zaburi 59:1-3 “Ee Mungu wangu, uniponye na adui zangu, Uniinue juu yao wanaoshindana nami. Uniponye nao wafanyao maovu, Uniokoe na watu wa damu. Kwa maana wanaiotea nafsi yangu; Wenye nguvu wamenikusanyikia; Ee Bwana, si kwa kosa langu, Wala si kwa hatia yangu.”

Mwandishi wa Zaburi hii Daudi anazungumza kwa lugha ya fumbo au lugha ya kimashairi akilinganisha maisha yake au nafsi yake kama maisha ya ndege, Ndege ni viumbe dhaifu sana na hawana nguvu ya kujitetea  na wala wengi hawajui kama wanawindwa au wana maadui, moyo wa ndege wengi ni moyo mwororo na mnyoofu ndege hawana neno na mtu wao wanapoamka asubuhi hawafikiri kufanya uadui na mtu, wao huamka na kumtukuza Mungu kisha kuendelea na majukumu yao ya kila siku, hawajui kama kuna mtu ataamka na kuwawekea mtego, wala hawajui kuwa kuna mtu ataamka na kuwageuza wao kuwa mfugo au kitoweo au kuwafungua katika tundu hawajui kama kuna wawindaji, ni muhimu ukaishi maisha yako lakini uwe makini na wawindaji, wawindaji wako kila mahali!

Lugha hii anayoitumia mwandishi wa Zaburi inawahusu watu wanaomcha Mungu, wengi wanawindwa nafsi zao lakini hawajui, wengi huamini kila mtu na wakati mwingine hawajui kama kuna mtu anaweza kuwa adui na kuziwinda nafsi zao, Ndege anawakilisha udhaifu wa mwanadamu, Hakuna mwanadamu mwenye nguvu ya kuvunja mitego ya adui Shetani na hata kujiokoa katika mikono yake, Shetani hutumia njia mbalimbali katika kuhakikisha kuwa unaingia kwenye mitego yake ikiwa ni pamoja na kuitumia hofu, magonjwa, dhambi, mauti,  na mashambulizi makali kutoka kwa majeshi yake ya pepo wabaya na watumishi wake wanadamu yaani maajenti wake, waganga, wachawi,  wanga, wenye hila na wenye wivu,Tunapoishi duniani fahamu na kuelewa kuwa wewe ni dhaifu kama ndege na bila masaada wa Mungu ni vigumu kwako kuwa huru kama Mungu mwenye nguvu hatakulinda na kukuepusha na mitego ya wawindaji, kila kitu duniani ulicho nacho kinawindwa, wewe hujui, ndoa yako inawindwa, kazi yako inawindwa, cheo chako kinawindwa, mali zako zinawindwa, biashara yako inawindwa, familia yako inawindwa, masomoni, unawindwa, huduma yako inawindwa, wawindaji ni watu wenye uchungu, ni wenye wivu, ni wenye nia mbaya, ni wenye hila na wamejaa kila mahali duniani, hata kwenye genge lako la nyanya pale sokoni, unawindwa, kama ndege katika mtego wa wawindaji, Bwana akupe neema kuigundua mitego yote unayotegewa na akuokoe na mitego ya wawaindaji katika jina la Yesu Kristo sema ameeeen!

Nafsi katika mitego ya wawindaji

Tumeona kuwa maisha ya mwanadamu ni kama maisha ya ndege katika mitego ya adui, na kinachowindwa katika maisha yetu mara tu baada ya kuzaliwa kwetu ni Nafsi, Neno nafsi katila lugha ya kiebrania ni “Nephesh” ambalo linamaanisha uhai, nafsi au mtu wa ndani, mwanadamu ana sehemu kuu tatu Mwili, Nafsi na Roho, vita vyetu vyote vya kiroho na kimaamuzi vinafanyika katika nafsi, nafsi inaponaswa katika mtego ambao unajulikana kama “Pach” Kiebrania ikimaanisha “tanzi”, au mbinu za kunasia, na wawindaji wanaitwa “Yagosh” Kiebrania yaani  watu wenye hila au wanasao kwa hila, wenye wivu, wenye uchungu, wasiopenda maendeleo yako, sasa nafsi inapokamatwa unaingizwa katika utumwa wa mwindaji na huwezi kuachiwa mpaka Mungu aingilie kati, mtu anapokuendea kwa mganga kukuroga maana yake anaitafuta nafsi yako aikamate na kuielekeza kule anakotaka yeye, nafsi yako ikikamatwa unaingia utumwani unamezwa ukiwa hai unapoteza uhuru uliokusudiwa na Mungu katika maisha yako!, unaona maisha yako ni kama yako gizani nafsi yako imekalishwa mahali penye giza, watu wamekufunga, umekuwa kama ndege katika tundu unafugwa badala ya kuwa na uhuru wako mpana wa asili uliokusudiwa na Mungu!

Zaburi 143:3-4 “Maana adui ameifuatia nafsi yangu, Ameutupa chini uzima wangu. Amenikalisha mahali penye giza, Kama watu waliokufa zamani. Na roho yangu imezimia ndani yangu, Moyo wangu ndani yangu umesituka.”

Adui wanapoipata nafsi yako kila kitu ndani yako na mali yako kinachukuliwa mateka na nafsi yako ndiyo inayoteseka, na maisha yako yanaharibiwa unatupwa chini, unawekwa kwenye giza na unakuwepo duniani lakini ni kama mtu aliyekufa, wawindaji wakiishika nafsi yako wanajivunia majivumo makubwa wanatamba kuwa wamekuweza na huwezi kufurukuta tena, wamekuweka kwenye kiganja, wokovu wako au ukombozi wako ni mpaka Bwana pekee aingilie kati, nafsi ikishikwa unakuwa mtumwa huwezi kufanya unalotaka wala huwezi kufanya mapenzi ya Mungu bali utafanya kile nafsi yako inakokukokota na adui zako wanakokupeleka, utasikia yule sisi tumemuweka kwenye kiganja ujue wameishika nafsi yako, Utasikia Bosi mimi haniambii kitu nimemuweka hapa! ahaa nafsi imeshikwa, Makahaba wanaoiba waume za watu huwa wanatafuta kuwashika nafsi, wakishawashika, mumeo harudi kwako kwa watai, fedha anapeleka huko, anapewa raha za ajabu na kupikiwa vizuri ili wewe usahau familia yako na umtese mkeo wako kwa nini changamoto nafsi ikishatekwa umetekwa maisha yako yote, ukitaka kumtumikisha mtu mshike nafsi yake, watu wengi wameshikwa na wanatumika wakati mwingine bila kupenda!

Farao alipowakamata Israel na kuwaweka kwenye tundu la utumwa nani angeweza kuwafungulia? Ni mpaka mwenye nguvu alipoingilia kati na kushughulika na adui ndipo Bwana alipowaweka huru! Ona  

Kutoka 15:6-13 “BWANA, mkono wako wa kuume umepata fahari ya uwezo, BWANA, mkono wako wa kuume wawaseta-seta adui. Kwa wingi wa ukuu wako wawaangusha chini wanaokuondokea, Wapeleka hasira yako, nayo huwateketeza kama mabua makavu. Kwa upepo wa mianzi ya pua yako maji yalipandishwa, Mawimbi yakasimama juu wima mfano wa chungu, Vilindi vikagandamana ndani ya moyo wa bahari. Adui akasema, Nitafuatia, nitapata, nitagawanya nyara, Nafsi yangu itashibishwa na wao; Nitaufuta upanga wangu, mkono wangu utawaangamiza. Ulivuma kwa upepo wako, bahari ikawafunikiza; Wakazama kama risasi ndani ya maji makuu. Ee BWANA, katika miungu ni nani aliye kama wewe? Ni nani aliye kama wewe, mtukufu katika utakatifu, Mwenye kuogopwa katika sifa zako, mfanya maajabu? Ulinyosha mkono wako wa kuume, Nchi ikawameza. Wewe kwa rehema zako umewaongoza watu uliowakomboa, Kwa uweza wako uliwaelekeza hata makao yako matakatifu

Unaona Israel waliposhikwa ni Bwana ndiye aliyekuja kuwatoa, leo ni siku ambayo kila ambaye ameshikilia nafsi yako anaiachia kwa mkono wa Bwana ulio hodari ulioonyooshwa katika jina la Yesu!

Nafsi yangu imeokoka kama ndege

Zaburi 124:6-8 “Na ahimidiwe Bwana; Asiyetutoa kuwa mawindo kwa meno yao. Nafsi yetu imeokoka kama ndege Katika mtego wa wawindaji, Mtego umevunjika, nasi tumeokoka.  Msaada wetu u katika jina la Bwana, Aliyezifanya mbingu na nchi.”

Mwandishi anaijua historia na mbinu ya adui kuwa anachikotafuta ni nafsi na anaelewa wazi kuwa nafsi inawindwa kama ndege na kuwa wenye hila huweka mitego yao ili kutunasa kama ndege na wokovu wako unaweza kuja kwa namna mbili aidha Mungu akuokoe usiwe mawindo, ASIYETUTOA KUWA MAWINDO KWA MENO YAO au kama umekamatika AUVUNJE MTEGO, Daudi anaonyesha kuwa kutokuingia katika mtego sio kwa sababu ya ujanja wetu bali kwa sababu ya ulinzi wa Mungu na kama umeingia katika mtego kutoka sio kwa uwezo wako bali mtego umevunjika na mtego huo hauvunjiki wenyewe ni kwa msaada wa Bwana, hii maana yake ni nini mwenye uwezo wa kuvunja nguvu za adui zetu ni Mungu aliyeziumba mbingu na nchi, Ni Mungu pake yake anayeweza kukuokoa na mauti, Ni Mungu peke yake anayeweza kukuokoa na dhambi, na ni Mungu pake yake anayeweza kumshinda Shetani kwa niaba yetu na ni yeye anayeweza kuwa msaada kwa nafsi zetu, na ndege akitoka mtegoni huwa harudi tena, mtegoni, Amani ya kweli inamkalia, furaha ya moyo inarudi mzigo wa utumwa unakuwa mwepesi kwa wokovu wake, ndege hawana mikono wanahitaji mkono wa Mungu, wanapowekwa tunduni hawawezi kutoka wenyewe mpaka mwenye huruma awafungulie, leo mwenye huruma ataifungua nasfi yako, mwenye huruma atakuepusha na mtego, wengine wamekamatwa na dini, wengine ulevi, wengine uraibu wa madawa ya kukevya na ukahaba lakini yuko anayeweza kukuweka huru, popote pale ambapo nafsi yako imeshikwa Yesu yuko tayari kukufungua.

Yohana 8:31-36 “Basi Yesu akawaambia wale Wayahudi waliomwamini, Ninyi mkikaa katika neno langu, mmekuwa wanafunzi wangu kweli kweli; tena mtaifahamu kweli, nayo hiyo kweli itawaweka huru. Wakamjibu, Sisi tu uzao wake Ibrahimu, wala hatujawa watumwa wa mtu wakati wo wote; nawe wasemaje, Mtawekwa huru? Yesu akawajibu, Amin, amin, nawaambia, Kila atendaye dhambi ni mtumwa wa dhambi. Wala mtumwa hakai nyumbani sikuzote; mwana hukaa sikuzote. Basi Mwana akiwaweka huru, mtakuwa huru kweli kweli.

Mathayo 11:28-30 “Njoni kwangu, ninyi nyote msumbukao na wenye kulemewa na mizigo, nami nitawapumzisha. Jitieni nira yangu, mjifunze kwangu; kwa kuwa mimi ni mpole na mnyenyekevu wa moyo; nanyi mtapata raha nafsini mwenu; kwa maana nira yangu ni laini, na mzigo wangu ni mwepesi.”

Mwandishi wa zaburi hii anaiona kazi ya kuingilia kati na kuisaidia nafsi ya mwanadamu ni ya Mungu na ni yeye anayestahili kuhimidiwa na kutukuzwa hakuna mwanadamu mwenye mchango wowote katika kazi ya ukombozi wa mwanadamu zaidi ya kuokolewa kwa neema, mwanadamu ni dhaifu sana bila Mungu, hila za shetani ziko kuishambilia nafsi ya kila mmoja wetu ili aimeze lakini Mungu kwa rehema zake ndiye anayeweza kuuvunja mtego wa adui zetu au kutufungulia na tukaruka zetu angani tukiwa huru kama ndege, kila mtu aliyeokolewa anapaswa kujua wazi kuwa ni kwa neema tu na ni kwa msaada wa Mungu tunaokolewa, Mungu amekusudia tuwe na uwanda mpana wa kuufurahia uwepo wake na sio kufungiwa kwenye tundu kama ndege asiye na uhuru, Shetani anatumia mitego iliyojificha kuliko mashambulizi ya wazi na ni Mungu peke yake anayeweza kukusaidia kwanza usiingie katika mtego wa adui na kuwa mawindo, pili kama umenaswa kuuvunja mtego ili uweze kuwa huru, Ndege hana nguvu yoyote ya kwake ya kumsaidia kujifungulia mtego, Lakini yuko anayeweza kututunza tusiingie mtegoni na kama umeingia anaweza kutufungulia!, Mpenzi je wewe uko katika hali ya namna gani Umenaswa? Au unataka kunaswa? Bwana akupe neema na kukuhurumia asikuache kuwa mawindo kwa meno yao nafsi yako iokoke kama ndege katika mtego wa wawindaji na mtego uliokukamata uvunjike katika jina la Yesu Kristo Mwana wa Mungu aliye hai haleluyaaaaaaaaaaa

Zaburi 124:6-8 “Na ahimidiwe Bwana; Asiyetutoa kuwa mawindo kwa meno yao. Nafsi yetu imeokoka kama ndege Katika mtego wa wawindaji, Mtego umevunjika, nasi tumeokoka.  Msaada wetu u katika jina la Bwana, Aliyezifanya mbingu na nchi.”

 

Na. Rev. Innocent Samuel Kamote

Mkuu wawajenzi mwenye Hekima