Mathayo
17:1-5 “Na baada ya siku sita Yesu akawatwaa Petro,
na Yakobo, na Yohana nduguye, akawaleta juu ya mlima mrefu faraghani; akageuka
sura yake mbele yao; uso wake ukang'aa kama jua, mavazi yake yakawa meupe kama
nuru. Na tazama, wakatokewa na Musa na Eliya, wakizungumza naye. Petro akajibu
akamwambia Yesu, Bwana, ni vizuri sisi kuwapo hapa; ukitaka, nitafanya hapa
vibanda vitatu, kimoja chako wewe, na kimoja cha Musa, na kimoja cha Eliya.
Alipokuwa katika kusema, tazama, wingu jeupe likawatia uvuli; na tazama, sauti
ikatoka katika lile wingu, ikasema, Huyu ni Mwanangu, mpendwa wangu,
ninayependezwa naye; msikieni yeye.”
Utangulizi.
Moja ya maneno ya msingi ambayo dunia
inapaswa kuyazingatia ni haya yaliyowahi kutamkwa na Mungu Baba mwenyewe katika
mlima wa ugeuko (transfiguration) mbele
ya Petro Yakobo na Yohana. Kauli hii ni moja ya kauli nzito sana katika Agano
jipya kwa sababu ni kauli yenye mamlaka kubwa nayomtambulisha Bwana wetu Yesu
Kristo kwa mamlaka kubwa ili kwamba wanadamu wote wamsikilize kumtii na
kumfuata Kauli hii imerejewa kwa msisitizo katika njili zile tatu zifananazo,
Mathayo, Marko na Luka.
Marko
9:2-7 “Hata baada ya siku sita Yesu akawatwaa
Petro, na Yakobo, na Yohana, akawaleta juu ya mlima mrefu faraghani, peke yao;
akageuka sura yake mbele yao; mavazi yake yakimeta-meta, meupe mno, jinsi asivyoweza
dobi duniani kuyafanya meupe. Wakatokewa na Eliya pamoja na Musa, nao walikuwa
wakizungumza na Yesu.Petro akajibu, akamwambia Yesu, Rabi, ni vizuri sisi
kuwapo hapa; na tufanye vibanda vitatu, kimoja chako wewe, kimoja cha Musa, na
kimoja cha Eliya. Maana, hakujua la kunena, kwa kuwa waliingiwa na hofu nyingi.
Kisha likatokea wingu, likawatia uvuli; sauti ikatoka katika lile wingu, Huyu
ni Mwanangu, mpendwa wangu, msikieni yeye.”
Luka
9:28-35 “Baada ya maneno hayo yapata siku nane,
aliwatwaa Petro na Yohana na Yakobo, akapanda mlimani ili kuomba. Ikawa katika
kusali kwake sura ya uso wake ikageuka, mavazi yake yakawa meupe,
yakimeta-meta. Na tazama, watu wawili walikuwa wakizungumza naye, nao ni Musa
na Eliya; walioonekana katika utukufu, wakanena habari za kufariki kwake
atakakotimiza Yerusalemu.Petro na wale waliokuwa pamoja naye walikuwa
wamelemewa na usingizi; lakini walipokwisha amka waliuona utukufu wake, na wale
wawili waliosimama pamoja naye. Ikawa hao walipokuwa wakijitenga naye, Petro alimwambia
Yesu, Bwana mkubwa, ni vizuri sisi kuwapo hapa; na tufanye vibanda vitatu;
kimoja chako wewe, na kimoja cha Musa, na kimoja cha Eliya; hali hajui
asemalo. Alipokuwa akisema hayo,
lilitokea wingu likawatia uvuli, wakaogopa walipoingia katika wingu hilo. Sauti
ikatoka katika wingu, ikisema, Huyu ni Mwanangu, mteule wangu, msikieni yeye.”
Injili zote tatu zifananazo (Synoptic Gospel) zimerekodi tukio hili
muhimu, lililoshuhudiwa na Petro, Yakobo na Yohana kwa sababu ya umuhimu wake
mkubwa ambao leo tutachukua muda kuutafakari na kuusisitiza kwa jamii ili kila
mtu duniani apate kusadiki ya kuwa Yesu ni mwana wa Mungu na kwamba yeye ndiye
njia na kweli na uzima na hakuna mwingine kabla yake na baada yake, umuhimu wa
tukio hili kwa mtazamo wangu hauko katika kubadilika sura kwa Yesu Kristo, wala
katika kutokewa na Musa na Eliya lakini uzito mkubwa wa tukio hili uko katika
sauti ile “Huyu ndiye Mwanangu, mpendwa,
msikieni yeye!”, tutajifunza somo hili HUYU
NDIYE MWANANGU MPENDWA MSIKIENI YEYE kwa kuzingatia vipengele muhimu vitatu
vifuatavyo:-
·
Maana ya
neno Msikieni yeye!
·
Umuhimu wa
Yesu Kristo kwa wanadamu.
·
Huyu ndiye
Mwanangu mpendwa msikieni yeye.
Maana
ya neno Msikieni yeye
Wote tutakuwa tunafahamu kuwa neno la
Kiebrania kuhusu kusikia linajulikana kama neno “SHEMA” maana yake katika kiingereza “hear” or “Listen” “understand” “Obey” or “take action”neno hili
lina uzito mkubwa sana katika maandiko ya Kiebrania sio kwaajili ya kusikia
sauti pekee bali kusikia, kutii na kutekeleza, neno hilo likifanyiwa kazi
kimsingi lina Baraka kubwa sana na lisipofanyiwa kazi linasababisha laana mikosi
na balaa, kwa hiyo kila Myahudi alisisitizwa kuwa na bidii katika kusikia,
utaisikiliza sauti ya Bwana Mungu wako, huu ulikuwa ni msisitizo wa kitorati
Kumbukumbu
6:3-5 “SIKIZA BASI, EE ISRAELI, ukaangalie
kuzitenda; upate kufanikiwa, mpate kuongezeka sana, kama Bwana, Mungu wa baba
zako, alivyokuahidi, katika nchi ijaayo maziwa na asali. Sikiza, Ee Israeli;
Bwana, Mungu wetu, Bwana ndiye mmoja. Nawe mpende Bwana, Mungu wako, kwa moyo
wako wote, na kwa roho yako yote, na kwa nguvu zako zote.”
Kutoka
19:5-6 “Sasa basi IKIWA MTAITII SAUTI YANGU kweli
kweli, na kulishika agano langu, hapo ndipo mtakapokuwa tunu kwangu kuliko
makabila yote ya watu; maana dunia yote pia ni mali yangu, nanyi mtakuwa kwangu
ufalme wa makuhani, na taifa takatifu. Hayo ndiyo maneno utakayowaambia wana wa
Israeli.”
Kumbukumbu
28:1-2 “Itakuwa UTAKAPOSIKIA SAUTI YA BWANA, Mungu
wako, kwa bidii, kutunza kuyafanya maagizo yake yote nikuagizayo leo, ndipo
Bwana, Mungu wako, atakapokutukuza juu ya mataifa yote ya duniani;na baraka
hizi zote zitakujilia na kukupata usikiapo sauti ya Bwana, Mungu wako.”
Kutoka
23:20-26 “Tazama, mimi namtuma malaika aende mbele
yako, ili akulinde njiani na kukupeleka mpaka mahali pale nilipokutengezea.
Jitunzeni mbele yake, mwisikize sauti yake; wala msimtie kasirani; maana,
hatawasamehe makosa yenu; kwa kuwa jina langu limo ndani yake. Lakini UKIISIKIZA
SAUTI yake kweli, na KUYATENDA YOTE ninenayo mimi; ndipo mimi nitakuwa ni adui
wa adui zako, na mtesi wa hao wakutesao. Kwa kuwa malaika wangu atatangulia
mbele yako, na kukufikisha kwenye Mwamori, na Mhiti, na Mperizi, na Mkanaani,
na Mhivi, na Myebusi; nami nitawakatilia mbali. Usiisujudie miungu yao, wala
kuitumikia; wala usitende mfano wa matendo yao; bali utaiangamiza kabisa, na
nguzo zao utazivunja vipande vipande. Nanyi mtamtumikia BWANA, Mungu wenu, naye
atakibarikia chakula chako, na maji yako; nami nitakuondolea ugonjwa kati yako.
Hapatakuwa na mwenye kuharibu mimba, wala aliye tasa, katika nchi yako; na
hesabu ya siku zako nitaitimiza.”
Kwa hiyo kama wanafunzi wa Biblia
utakuwa umegundua kuwa neno kusikia, sikia, msikilizeni, tiini, linaambatana na
baraka kubwa sana ulimwenguni, endapo watu wa Mungu watajifunza na kuelewa kuwa
kusikia, kuna maana ya kutii, kutunza, kufanya, kuishi, kuamini na kufuata na
ndani ya neno hili kuna siri kubwa sana ya Baraka za Mungu ni kama Baraka zote
zimefungwa katika kusikiliza kunakotajwa kimaandiko yaani SHEMA basi kumsikia Yesu ni Baraka.
Kwa hiyo Sauti ya Mungu Baba
iliposikika kwa Petro, Yakobo na Yohana Huyu ndiye mwanangu mpendwa msikieni
yeye, wanafunzi hawa wa Yesu Kristo kwa kuwa walikuwa Wayahudi walikuwa na
uelewa mpana wa kile ambacho mbingu zilikuwa zinakimaanisha kuhusu Yesu Kristo,
mwanaye ni kwamba uko ulazima au amri kuwa yeye ni wa kuaminiwa, yeye ndiye wa
kumtii, yeye ndiye wa kumfuata, yeye ndiye wa kumtegemea, yeye ndiye wa
kusikilizwa, yeye ndiye wa kufuata maagizo yake yeye ndiye wa kutekeleza
asemayo na hakuna mwingine kabla yake wala baada yake, Ni lazima wafuate
mafundisho yake na kwa kumtii yeye Baraka zote zilizoahidiwa katika maandiko
zitatufuata
Umuhimu
wa Yesu Kristo kwa wanadamu.
Mathayo
17:1-5 “Na baada ya siku sita Yesu akawatwaa Petro,
na Yakobo, na Yohana nduguye, akawaleta juu ya mlima mrefu faraghani; akageuka
sura yake mbele yao; uso wake ukang'aa kama jua, mavazi yake yakawa meupe kama
nuru. Na tazama, wakatokewa na Musa na Eliya, wakizungumza naye. Petro akajibu
akamwambia Yesu, Bwana, ni vizuri sisi kuwapo hapa; ukitaka, nitafanya hapa
vibanda vitatu, kimoja chako wewe, na kimoja cha Musa, na kimoja cha Eliya.
Alipokuwa katika kusema, tazama, wingu jeupe likawatia uvuli; na tazama, sauti ikatoka
katika lile wingu, ikasema, Huyu ni Mwanangu, mpendwa wangu, ninayependezwa
naye; MSIKIENI yeye.”
Tukio hili katika maandiko ni tukio la
kipekee lisiloweza kusahaulika, Petro katika maisha yake yote aliweza
kumtumikia Mungu kwa jina la Yesu na hata miaka mingi sana ilipopita bado
aliendelea kulikumbuka tukio hili lililokuwa limemfunua Yesu Kristo katika
ubora wake na kama Bwana aliyekubalika kwa mamlaka kubwa zaidi kuliko yeyote
yule, hata wale walioheshimika sana katika jamii ya Israel kama Musa na Eliya akam
manabii wakubwa na muhimu sana, Petro hata alipokuwa anakaribia kufa bado alikumbuka
tukio lile la kipekee, la kufunuliwa kwa heshima na utukufu na kuthibitishiwa
ukuu wa Yesu Kristo kuliko manabii wote, kulikofanywa na Mungu Baba:-
2Petro
1:16-18 “Maana hatukufuata hadithi zilizotungwa kwa
werevu, tulipowajulisha ninyi nguvu zake Bwana wetu Yesu Kristo na kuja kwake;
bali tulikuwa tumeuona wenyewe ukuu wake. Maana alipata kwa Mungu Baba heshima
na utukufu, hapo alipoletewa sauti iliyotoka katika utukufu mkuu, Huyu ni
Mwanangu, mpendwa wangu, ninayependezwa naye. NA SAUTI HIYO SISI TULIISIKIA ikitoka
mbinguni tulipokuwa pamoja naye katika mlima ule mtakatifu”.
Mungu alitaka Petro, Yakobo na Yohana
na walimwengu wote baada yao, kuwa na uelewa huu mkubwa kuhusu Yesu Kristo ili
asitokee mtu akamvunjia Yesu Heshima, Yesu ni mkuu na mbora kuliko nabii Musa,
Eliya na wengine wote, sio tu kuwa torati na manabii zilizungumza habari zake
lakini hata Mungu Baba mwenyewe alithibitisha habari zake na kina Petro
waliisikia sauti, iliyowathibitishia kuwa sifa za Yesu sio hadithi za kutungwa
kwa werevu bali ni uthibitisho kutoka mbinguni kuwa Yesu ni mwana wa Mungu na
ulimwengu unapaswa kumuamini yeye na kumtii;-
-
Maandiko
yote yanaelekeza kwa Yesu Kristo – Unapoyachambua maandiko yote kutoka
agano la kale mpaka mwisho kuanzia Torati na manabii wote walielekeza watu kwa
Yesu Kristo na ukiona nabii anaelekeza watu kwa mtu mwingine na sio Kristo huyo
ni nabii wa uongo, au ukiona nabii anaelekeza watu wamwamini yeye na sio Yesu
Kristo basi huyo ni nabii wa uongo, Yesu Kristo ndio ufunuo wa mwisho wa Mungu
kwa wanadamu wote.
Luka 24:25-31 “Akawaambia, Enyi
msiofahamu, wenye mioyo mizito ya kuamini yote waliyoyasema manabii! Je!
Haikumpasa Kristo kupata mateso haya na kuingia katika utukufu wake? Akaanza
kutoka Musa na manabii wote, akawaeleza katika maandiko yote mambo yaliyomhusu
yeye mwenyewe. Wakakikaribia kile kijiji walichokuwa wakienda, naye alifanya
kama anataka kuendelea mbele.Wakamshawishi wakisema, Kaa pamoja nasi, kwa kuwa
kumekuchwa, na mchana unakwisha. Akaingia ndani kukaa nao. Ikawa alipokuwa
ameketi nao chakulani, alitwaa mkate, akaubariki, akaumega, akawapa.
Yakafumbuliwa macho yao, wakamtambua; kisha akatoweka mbele yao.”
-
Musa ingawa alikuwa nabii mkubwa
lakini aliwaelekeza watu kwa Yesu – Na kuamuru watu wote wamsikilize
yeye yaani wamwamini, wamtii na kuyashika mafundisho yake, mtu awaye yote
ambaye hatamsikiliza atakufa
Kumbukumbu 18:15-18 “Bwana, Mungu wako,
atakuondokeshea nabii miongoni mwa ndugu zako kama nilivyo mimi; MSIKILIZENI
YEYE. Kama vile ulivyotaka kwa Bwana, Mungu wako, huko Horebu, siku ya
kusanyiko, ukisema, Nisisikie tena sauti ya Bwana, Mungu wangu, wala nisiuone
tena moto huu mkubwa, nisije nikafa. Bwana akaniambia, Wametenda vema kusema
walivyosema. Mimi nitawaondokeshea nabii miongoni mwa ndugu zao mfano wako
wewe, nami nitatia maneno yangu kinywani mwake, naye atawaambia yote
nitakayomwamuru.”
Matendo 3:22-24 “Kwa maana Musa kweli
alisema ya kwamba, Bwana Mungu wenu atawainulieni nabii, katika ndugu zenu,
kama MIMI; MSIKIENI YEYE katika mambo yote atakayonena nanyi. Na itakuwa ya
kwamba kila mtu ASIYEMSIKILIZA NABII HUYO ATAANGAMIZWA na kutengwa na watu
wake. Naam, na manabii wote tangu Samweli na wale waliokuja baada yake, wote
walionena, walihubiri habari za siku hizi.”
-
Isaya alimuhubiri Kristo – Isaya alijulikana kama muhubiri mkubwa
sana wa nyakati za agano la kale watu wengi wanamuita nabii wa Masihi au
mwinjilishi wa agano la kale yeye alipewa neema ya kutoa unabii ulio wazi sana
kuhusu Yesu Kristo ikiwepo mamlaka yake, kuzaliwa kwake na mateso yake
akimuelezea Kristo miaka 700 kabla yake kwa uweza wa ajabu sana Isaya
alimuhubiri Kristo na kumtaja kama mshauri wa ajabu, Mungu mwenye nguvu, baba
wa milele na mfalme wa Amani, sasa utapata wapi uzima na uponyaji na wokovu
kama humsikilizi?
Isaya 7:14 “Kwa hiyo Bwana
mwenyewe atawapa ishara. Tazama, bikira atachukua mimba, atazaa mtoto
mwanamume, naye atamwita jina lake Imanueli.”
Isaya 9:6 “Maana kwa ajili yetu
mtoto amezaliwa, Tumepewa mtoto mwanamume; Na uweza wa kifalme utakuwa begani
mwake; Naye ataitwa jina lake, Mshauri wa ajabu, Mungu mwenye nguvu, Baba wa
milele, Mfalme wa amani.”
Isaya 53:1-9 “Ni nani aliyesadiki
habari tuliyoileta? Na mkono wa Bwana amefunuliwa nani? Maana alikua mbele zake
kama mche mwororo, Na kama mzizi katika nchi kavu; Yeye hana umbo wala uzuri;
Na tumwonapo hana uzuri hata tumtamani. Alidharauliwa na kukataliwa na watu;
Mtu wa huzuni nyingi, ajuaye sikitiko; Na kama mtu ambaye watu humficha nyuso
zao, Alidharauliwa wala hatukumhesabu kuwa kitu.Hakika ameyachukua masikitiko
yetu, Amejitwika huzuni zetu; Lakini tulimdhania ya kuwa amepigwa, Amepigwa na
Mungu, na kuteswa. Bali alijeruhiwa kwa makosa yetu, Alichubuliwa kwa maovu
yetu; Adhabu ya amani yetu ilikuwa juu yake, Na kwa kupigwa kwake sisi
tumepona.Sisi sote kama kondoo tumepotea; Kila mmoja wetu amegeukia njia yake
mwenyewe; Na Bwana ameweka juu yake Maovu yetu sisi sote.Alionewa, lakini
alinyenyekea, Wala hakufunua kinywa chake; Kama mwana-kondoo apelekwaye
machinjoni, Na kama vile kondoo anyamazavyo Mbele yao wakatao manyoya yake;
Naam, hakufunua kinywa chake. Kwa kuonewa na kuhukumiwa aliondolewa; Na maisha
yake ni nani atakayeisimulia? Maana amekatiliwa mbali na nchi ya walio hai;
Alipigwa kwa sababu ya makosa ya watu wangu. Wakamfanyia kaburi pamoja na
wabaya; Na pamoja na matajiri katika kufa kwake; Ingawa hakutenda jeuri, Wala
hapakuwa na hila kinywani mwake.”
-
Yohana mbatizaji alimuhubiri
Kristo na kuonyesha kuwa ni mwenye mamlaka kuu – Yohana 1:26-30 “Yohana
akawajibu akisema, Mimi nabatiza kwa maji. Katikati yenu amesimama yeye
msiyemjua ninyi. Ndiye yule ajaye nyuma yangu, ambaye mimi sistahili kuilegeza
gidamu ya kiatu chake. Hayo yalifanyika huko Bethania ng'ambo ya Yordani,
alikokuwako Yohana akibatiza. Siku ya pili yake amwona Yesu anakuja kwake,
akasema, TAZAMA, MWANA-KONDOO WA MUNGU, aichukuaye dhambi ya ulimwengu! Huyu
ndiye niliyenena habari zake ya kwamba, Yuaja mtu nyuma yangu, ambaye amekuwa
mbele yangu; kwa maana alikuwa kabla yangu.”
Yohana 3:26-31 “Wakamwendea Yohana,
wakamwambia, Rabi, yeye aliyekuwa pamoja nawe ng'ambo ya Yordani, yeye
uliyemshuhudia, tazama, huyo anabatiza na watu wote wanamwendea.Yohana akajibu,
akasema, Hawezi mtu kupokea neno lo lote isipokuwa amepewa kutoka mbinguni.
Ninyi wenyewe mwanishuhudia ya kwamba nalisema, Mimi siye Kristo, bali
nimetumwa mbele yake. Aliye naye bibi arusi ndiye bwana arusi; lakini rafiki
yake bwana arusi, yeye anayesimama na kumsikia, aifurahia sana sauti yake bwana
arusi. Basi hii furaha yangu imetimia. Yeye hana budi kuzidi, bali mimi
kupungua. Yeye ajaye kutoka juu, huyo yu juu ya yote. Yeye aliye wa dunia,
asili yake ni ya dunia, naye anena mambo ya duniani. Yeye ajaye kutoka mbinguni
yu juu ya yote.”
-
Daudi – alihubiri na kutabiri kwa kina
sana kwa habari ya mambo mengi kuhusu Yesu Kristo, na alimuita Bwana na
kutabiri swala zima la kuketi katika mkono wa kuume wa Mungu huko mbinguni ona
:-
Zaburi 110:1-2 “Neno la Bwana kwa
Bwana wangu, Uketi mkono wangu wa kuume, Hata niwafanyapo adui zako Kuwa chini
ya miguu yako. Bwana atainyosha toka Sayuni Fimbo ya nguvu zako. Uwe na enzi
kati ya adui zako;”
Mathayo 22:41-46 “Na Mafarisayo
walipokusanyika, Yesu aliwauliza, akisema, Mwaonaje katika habari za Kristo? Ni
mwana wa nani? Wakamwambia, Ni wa Daudi. Akawauliza, Imekuwaje basi Daudi
katika Roho kumwita Bwana, akisema, Bwana alimwambia Bwana wangu, Uketi mkono
wangu wa kuume, Hata niwawekapo adui zako Kuwa chini ya miguu yako? Basi, Daudi
akimwita Bwana, amekuwaje ni mwanawe? Wala hakuweza mtu kumjibu neno; wala
hakuthubutu mtu ye yote tangu siku ile kumwuliza neno tena.”
-
Paulo mtume alimuelezea Yesu kwa
kina sana - Wafilipi 2:5-11 “Iweni na nia iyo hiyo ndani yenu ambayo ilikuwamo
pia ndani ya Kristo Yesu; ambaye yeye mwanzo alikuwa yuna namna ya Mungu, naye
hakuona kule kuwa sawa na Mungu kuwa ni kitu cha kushikamana nacho; bali
alijifanya kuwa hana utukufu, akatwaa namna ya mtumwa, akawa ana mfano wa
wanadamu; tena, alipoonekana ana umbo kama mwanadamu, alijinyenyekeza akawa
mtii hata mauti, naam, mauti ya msalaba. Kwa hiyo tena Mungu alimwadhimisha
mno, akamkirimia Jina lile lipitalo kila jina; ili kwa jina la Yesu kila goti
lipigwe, la vitu vya mbinguni, na vya duniani, na vya chini ya nchi; na kila
ulimi ukiri ya kuwa YESU KRISTO NI BWANA, kwa utukufu wa Mungu Baba.”
Kila muhubiri nyakati za kanisa
la kwanza alimuhubiri Kristo, kujulikana kwetu, kuheshimika kwetu hakutakuja
kwa sababu ya kujijengea jina kutakuja kama tunamuinua Yesu Kristo katika
maisha yetu na mahubiri yetu, kazi ya kila mtumishi wa Mungu ni kuwaelekeza
watu wa Mungu kwa Yesu Kristo, nje ya Yesu Kristo huwezi kupata matokeo
yanayokusudiwa, Mungu aliyemthibitisha Yesu kwa wanafunzi wake hawezi
kumthibitisha kwa wasiomsikiliza au kumtii, kama tunataka kuona matokeo makubwa
sana katika injili basi tumuhubiri Yesu Kristo:-
Filipo aliposhuka Samaria alimuhubiri Kristo na watu
waliposikia waliponywa na kufunguliwa na kuokolewa - Matendo 8:5-8. “Filipo
akatelemka akaingia mji wa Samaria, AKAWAHUBIRI KRISTO. Na makutano kwa nia
moja WAKASIKILIZA maneno yale yaliyosemwa na Filipo walipoyasikia na kuziona
ishara alizokuwa akizifanya. Kwa maana pepo wachafu wakawatoka wengi
waliopagawa nao, wakilia kwa sauti kuu; na watu wengi waliopooza, na viwete,
wakaponywa. Ikawa furaha kubwa katika mji ule.”
-
Ni Yesu Kristo pekee ndiye mwenye
maneno ya uzima wa milele – watu wengi wanaweza kuwa na maneno ya Hekima “Falasafa”,
lakini maneno hayo hayana uwezo wa kutoa uzima huu wala wa milele Yesu Kristo
anayo maneno ya uzima wa milele, kila mtu anayemsikiliza anapewa uwezo wa kuwa
na uzima wa milele
Yoahan 6:68-69 “Basi Simoni Petro
akamjibu, Bwana! Twende kwa nani? Wewe unayo maneno ya uzima wa milele.Nasi
tumesadiki, tena tumejua, ya kuwa wewe ndiwe Mtakatifu wa Mungu.”
-
Ni Yesu Kristo pekee ambaye anatajwa kuwa ndio njia na
kweli na uzima, Mungu anataka watu wasimsikilize mwingine bali wamsikilize Yesu
kwani wakimsikiliza yeye hawatapotea, Mungu hataki wanadamu wasikilize njia
nyingine zinazopingana na Kristo au kuwaongoza kwenda upotevuni. Unataka uzima
mwamini Bwana Yesu, mtii.
Yohana 14:6 “Yesu
akamwambia, Mimi ndimi njia, na kweli, na uzima; mtu haji kwa Baba, ila kwa
njia ya mimi.”
-
Ni Yesu Kristo pekee ambaye amepewa mamlaka yote mbinguni
na Duniani. Na jina kubwa kuliko majina yote iwe ni ya mbinguni au duniani
uwezi kumfananisha Yesu Kristo na nabii mwingine yeyote, yeyote.
Mathayo 28:18 “Yesu akaja kwao,
akasema nao, akawaambia, Nimepewa mamlaka yote mbinguni na duniani.”
Wafilipi 2:9-11 “Kwa hiyo tena Mungu
alimwadhimisha mno, akamkirimia Jina lile lipitalo kila jina; ili kwa jina la
Yesu kila goti lipigwe, la vitu vya mbinguni, na vya duniani, na vya chini ya
nchi; na kila ulimi ukiri ya kuwa YESU KRISTO NI BWANA, kwa utukufu wa Mungu
Baba.”
Huyu
ndiye Mwanangu mpendwa msikieni yeye.
Mathayo
17:1-5 “Na baada ya siku sita Yesu akawatwaa Petro,
na Yakobo, na Yohana nduguye, akawaleta juu ya mlima mrefu faraghani; akageuka
sura yake mbele yao; uso wake ukang'aa kama jua, mavazi yake yakawa meupe kama
nuru. Na tazama, wakatokewa na Musa na Eliya, wakizungumza naye. Petro akajibu
akamwambia Yesu, Bwana, ni vizuri sisi kuwapo hapa; ukitaka, nitafanya hapa
vibanda vitatu, kimoja chako wewe, na kimoja cha Musa, na kimoja cha Eliya.
Alipokuwa katika kusema, tazama, wingu jeupe likawatia uvuli; na tazama, sauti
ikatoka katika lile wingu, ikasema, Huyu ni Mwanangu, mpendwa wangu,
ninayependezwa naye; MSIKIENI yeye.”
Wakati Mungu anasema maneno haya ya
muhimu sana mapema katika tukio hilo, Musa na Eliya walikuwa wameonekana wakizungumza
na Yesu akiwa katikati yao, kimsingi Musa anawakilisha Sheria au Torati na
Eliya anawakilisha Manabii, Katika hali ya sintofahamu Petro alitoa ushauri
ambao Mbingu ziliukataa na kutamka maneno hayo mazito, Petro alisema ni vema wakikaa hapo na vikajengwa
vibanda vitatu kimoja cha Kristo, kingine cha Musa na kingine cha Eliya, unajua
ni kwanini Petro alitamka haya katika mawazo yake alifikiri kuwa Musa na Eliya
wako sawasawa na Yesu na hapo ndipo Mungu alipoingilia kati kumjulisha Petro na
wenzake kuwa manabii hao ni tofauti na Bwana Yesu “HUYU NDIYE MWANANGU MPENDWA NINAYEPENDEZWA NAYE MSIKIENI YEYE”
maneno haya yalikuwa yanafunua uwazi wa Mungu Baba kuwa Yesu ni mkuu kuliko
Musa, Yesu ni mkuu kuliko Eliya, Yesu ni zaidi ya manabii wote, Yesu ndiye
utimilifu wa Sheria na manabii, kwa hiyo yeye ndiye wa kusikilizwa, yeye ndiye
wa kuaminiwa, yeye ndiye wa kumtii, yeye ndiye wa kufuata yeye ndiye wa
kuyashika mafundisho yake, yeye ndiye mtekeleze maagizo yake, yeye ndiye wa
kutegemewa, kumlinganisha Yesu na Musa ni sawa na kumlinganisha mtimishi
mwaminifu na Mwana mwaminifu katika nyumba ya Mungu.
Waebrania
3:3-6 “Kwa maana huyo amehesabiwa kuwa amestahili
utukufu zaidi kuliko Musa, kama vile yeye aitengenezaye nyumba alivyo na
heshima zaidi ya hiyo nyumba. Maana kila nyumba imetengenezwa na mtu; ila yeye
aliyevitengeneza vitu vyote ni Mungu. Na Musa kweli alikuwa mwaminifu katika
nyumba yote ya Mungu kama mtumishi, awe ushuhuda wa mambo yatakayonenwa
baadaye; bali Kristo, kama mwana, juu ya nyumba ya Mungu; ambaye nyumba yake ni
sisi, kama tukishikamana sana na ujasiri wetu na fahari ya taraja letu mpaka
mwisho.”
Kwa msingi huo mtu awaye yote ambaye
hatamsikiliza Yesu Kristo huyo atakatiliwa mbali na watu wake, ataangamia
Matendo
3:22-23 “Kwa maana Musa kweli alisema ya kwamba,
Bwana Mungu wenu atawainulieni nabii, katika ndugu zenu, kama mimi; msikieni
yeye katika mambo yote atakayonena nanyi.Na itakuwa ya kwamba kila mtu
asiyemsikiliza nabii huyo ataangamizwa na kutengwa na watu wake.”
Kwa hiyo maneno HUYU NDIYE MWANANGU MPENDWA NINAYEPENDEZWA NAYE MSIKILIZENI YEYE Ni tamko la mamlaka ya kimbinguni linalomtangaza
Yesu Kristo kuwa ndiye Masihi na Mwokozi wa ulimwengu na hakuna nabii mwingine
yeyote ambaye ni mkubwa au ana heshima kubwa kuliko yeye tena wala hakuna
mbadala wake, huyu ndiye Alfa na Omega kwa hiyo wito huo haukuwa wa Petro,
Yakobo na Yohana bali ulikuwa ni wito kwa ulimwengu mzima kwamba macho na
masikio yetu, mioyo yetu, imani yetu na utii wetu uelekezwe kwa Yesu, Musa
alielekeza watu kwa Yesu, Manabii wote walielekeza kwa Yesu, Mitume
walimuhubiri Kristo, na Roho Mtakatifu anamshuhudia Kristo, kwa hiyo hili
lilikuwa onyo pia la wazi kwa wanadamu kwamba ole wako umwanimi mwingine au
atakayekuja nyuma ya Yesu na kujifanya ni nabii au mjumbe wa mwenyezi Mungu, ni
ujumbe unaowasaidia wakristo kutambua wazi nani ni nabii wa kweli na nani ni
nabii wa uongo. Ole wako umuhubiri Siddhartha
Gautama Budha wa Budha, ole wako
umuhubiri Guru Nanak wa Sikhism, Ole wako umuhubiri Lao Tzu wa Taoisim, Ole wako Umuhubiri Master
Confucius, wa Confucianism, Ole
wako umuhubiri Zoroaster wa Zoroastrianism, Ole wako umuhubiri Bahaulah wa Bahai, Ole wako umuhubiri Muhamad
wa Uislamu, mitume na watumishi wa
Mungu wa kweli wanamuhubiri Kristo, sisi tunamuhubiri Yesu Kristo ya kuwa ni
Bwana, ni hatari sana kumlinganisha Yesu na wanafalasafa wengine duniani.
2Wakorintho
4:3-5 “Lakini ikiwa injili yetu imesitirika, imesitirika
kwa hao wanaopotea; ambao ndani yao mungu wa dunia hii amepofusha fikira zao
wasioamini, isiwazukie nuru ya injili ya utukufu wake Kristo aliye sura yake
Mungu. Kwa maana hatujihubiri wenyewe, bali Kristo Yesu ya kuwa ni Bwana; na
sisi wenyewe kuwa tu watumishi wenu kwa ajili ya Yesu.”
Na
Rev. Innocent Samuel Kamote
Mkuu wa wajenzi mwenye Hekima.
.jpg)
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni