Zaburi 42:1-4 “Kama ayala aioneavyo shauku mito ya maji. Vivyo hivyo nafsi yangu inakuonea shauku, Ee Mungu. Nafsi yangu inamwonea kiu MUNGU, Mungu aliye hai, Lini nitakapokuja nionekane mbele za Mungu? Machozi yangu yamekuwa chakula changu mchana na usiku, Pindi wanaponiambia mchana kutwa, Yuko wapi Mungu wako. Nayakumbuka hayo nikiweka wazi nafsi yangu ndani yangu, Jinsi nilivyokuwa nikienda na mkutano, Na kuwaongoza nyumbani kwa Mungu, Kwa sauti ya furaha na kusifu, mkutano wa sikukuu.”
Utangulizi:
Kila mwanadamu aliyeumbwa na
Mungu katika roho yake ameumbiwa kiu, njaa, hamu na shauku ya kutaka kuwa na uhusiano
na Mungu, kimsingi mwanadamu aliumbwa ili awe na ushirika au uhusiano na Mungu,
ushirika huo au uhusiano huo unafananishwa na kiu ya maji aliyonayo Ayala, hii
ni kiu ya uhitaji wa uwepo wa Mungu, kiu ya kutaka kumsikia Mungu, kiu ya
kutaka kumuabudu, kiu ya kutaka kumtumikia Mungu katika viwango vyenye kuleta
utoshelevu, kiu ya kutaka kuongozwa na yeye na kumuona Mungu akitembea katika
utukufu wake, Kama kuna jambo linaumiza moyo wa mtu aliyezoea kuwa na ushirika
na Mungu ni pamoja na kutokuhisi ule uwepo wake, Musa alikuwa na kiu na shauku
ya kutaka uwepo wa Mungu uwe pamoja naye kiasi kwamba alimwambia Mungu uso wako
usipokwenda pamoja nasi usituchukue kutoka hapa, hii ilikuwa ni shauku ya
kuhitaji uwepo wa Mungu kama jambo la lazima, aliona bila uwepo wa Mungu yeye
na wana wa Israel hawawezi lolote.
Kutoka 33:13-15 “Basi, sasa nakuomba, ikiwa
nimepata neema mbele zako, unionyeshe njia zako, nipate kukujua, ili nipate
neema mbele zako; ukakumbuke ya kuwa taifa hilo ndilo watu wako. Akasema, Uso
wangu utakwenda pamoja nawe, nami nitakupa raha. Naye akamwambia, Uso wako
usipokwenda pamoja nami, usituchukue kutoka hapa.”
Mwandishi wa zaburi hii ya “42” ambaye
kitaalamu ni wana wa Kora waliitumia zaburi hii ambayo iko katika kundi la zaburi
za Kuomboleza, yaani za mwandishi anaomboleza kwamba hawezi tena kwenda
Hekaluni nyakati za sikukuu mbalimbali, kutokana na mazingira kumtenga
asikaribie uwepo wa Mungu, Mwandishi anatumia hapo mfano wa Ayala (Kulungu) kuonyesha
jinsi ambayo nasfi yao ilivyo na shauku na kiu ya kutaka maji, Nao wana wa Kora
wana kiu ya kuona uwepo wa Mungu, yaani wana kiu na shauku ya uwepo wa Mungu. Lakini
wako katika mazingira magumu ambapo kuabudu kwao sio kwa furaha na uhuru kama
vile kwenda Hekaluni, kiu hii ya kuutafuta uwepo wa Mungu hekaluni mwake
inatupa fursa ya kuitafakari zaburi hii chini ya kichwa Nafsi yangu inakuonea kiu kama Ayala! Na tutajifunza somo hili kwa
kuzingatia vipengele vitatu vifuatavyo:-
·
Kwa nini
kiu kama Ayala?.
·
Nafsi
yangu inakuonea kiu kama Ayala.
·
Umuhimu
wa kuwa na kiu kama Ayala.
Kwa nini kiu kama Ayala?
Zaburi 42:1-2 “Kama ayala aioneavyo shauku
mito ya maji. Vivyo hivyo nafsi yangu inakuonea shauku, Ee Mungu. Nafsi yangu
inamwonea kiu MUNGU, Mungu aliye hai, lini nitakapokuja nionekane mbele za
Mungu?”
Mwandishi yaani wana wa Kora
wakiimba kwa niaba ya Daudi, wanaonyesha kiu kubwa sana ya kutamani kwenda
nyumbani mwa Bwana ili kujihudhurisha mbele za Mungu, akitaka kuielezea kiu
yake na hamu na shauku ya kutaka kuutafuta uwepo wa Mungu mwandishi anatumia
mfano wa Ayala atamanivyo maji ya
mto sawa na kiu yake ya kumtafuta Mungu, Mwandihi hakuchagua mfano huu kwa
bahati tu lakini bila shaka alikuwa na ujuzi mkubwa kuhusu mnyama huyu Ayala au (Kulungu) Katika lugha ya Kiebrania mnyama huyu anaitwa ‘ayรขl
sawa na neno Ayala la Kiswahili
na Deer la kiingereza jina lingine
la Kiswahili ni Kulungu, au paa, ingawa paa wako wa aina nyingi sana!
Ayala au Paa ni mnyama
anayejulikana sana kuwa ni rahisi sana
kushambuliwa na wanyama wakali, na kwa sababu hiyo kwaajili ya kujilinda wao huishi
katika maeneo ya milimani hasa katika mbuga za wanyama jangwani au nyikani na
pia wana uwezo wa kukimbia kwa umbali mrefu kwa kasi, kutokana na uwezo wake wa
kukimbia kwa kasi kati ya 35-40 mph huku
akiruka ruka uwezo wake wa kuruka ruka ni kati ya 8-10 futi sana yeye hutumia nguvu ambazo zinapoteza maji mwilini
mwake kwa haraka, kwa hiyo hujikuta akisumbuliwa sana na kiu, na kwa sababu
hiyo hawezi kutulia ni lazima atafute maji bila kuacha,Mwili wa Ayala umeumbwa
kwa maji kwa asilimia 65% kwa hivyo
hata kama kuna chakula cha kutosha Maji yana umuhimu mkubwa sana kwake
vinginevyo hataweza kuwa na nguvu za kukimbia maadui zake, lakini pia hawezi
kuishi muda mrefu bila maji kwa hiyo uhai wake unategemeana sana na kunywa
maji, sio hivyo tu maisha yake juani na jangwani na kwenye joto huchangia
kuifanya kiu yake kuwa kali kuliko wanyama wa kawaida, kwa hiyo hawezi kuishi
bila maji, maji kwake ni hitaji lisilozuilika, maji kwake ni uhai, maji kwake
ni ya lazima, maji kwake ni swala la dharula kwa hiyo wana wa Kora wanatumia
mfano wa Ayala kuonyesha kuwa wao nao uwepo wa Mungu una umuhimu mkubwa sana
sawa tu na Ayala anavyohitaji maji ya mito kwa kunywa!
Zaburi 63:1-3 “Ee MUNGU, Mungu wangu,
nitakutafuta mapema, Nafsi yangu inakuonea kiu, Mwili wangu wakuonea shauku,
Katika nchi kame na uchovu, isiyo na maji.Ndivyo nilivyokutazama katika
patakatifu, Nizione nguvu zako na utukufu wako. Maana fadhili zako ni njema
kuliko uhai; Midomo yangu itakusifu.”
Nafsi yangu inakuonea kiu kama Ayala.
Kwa nini Mwandishi alikuwa na kiu
hii inayofananishwa na kiu ya Ayala? Mwandishi anaonekana kuwa alikuwa katika kipindi
cha shida na taabu, alikuwa amefukuzwa mbali na nyumba ya Bwana, kwa hiyo hakuwa
na Muda wa kujiudhurisha mbele za Mungu na badala yake alikuwa akikimbia kutoka
nyika moja kwenda nyika nyingine, alikuwa katika mashambulizi makali, hali
ngumu na kipindi cha giza la kiroho, kwa hiyo alihisi maisha yake yako hatarini
na uwepo wa Mungu pekee ndio ulinzi wake na hata ingawa alimtegema Mungu adui
zake waliohoji yuko wapi Mungu wake, mwandishi alikuwa akitoa machozi usiku na
mchana na machozi yakawa kama chakula chake!
Zaburi 42:3-6 “Machozi yangu yamekuwa
chakula changu mchana na usiku, Pindi wanaponiambia mchana kutwa, Yuko wapi
Mungu wako. Nayakumbuka hayo nikiweka wazi nafsi yangu ndani yangu, Jinsi
nilivyokuwa nikienda na mkutano, Na kuwaongoza nyumbani kwa Mungu, Kwa sauti ya
furaha na kusifu, mkutano wa sikukuu. Nafsi yangu, kwa nini kuinama, Na
kufadhaika ndani yangu? Umtumaini Mungu; Kwa maana nitakuja kumsifu, Aliye afya
ya uso wangu, Na Mungu wangu. Nafsi yangu imeinama ndani yangu, kwa hiyo
nitakukumbuka, Toka nchi ya Yordani, na Mahermoni, na toka kilima cha Mizari.”
Unaona anakumbuka alivyokuwa
akiongoza watu kwenda nyumbani mwa Bwana kwa furaha, lakini siku hizo zimetoweka,
yuko mbali na uwepo wa Mungu anakaukiwa kwa hiyo kiu yake kwa Mungu iliongezeka
kwa sababu ya mazingira magumu aliyokuwa anayapitia, sasa hafurahii uwepo wa
Mungu kama zamani kwa sababu yuko mbali, yuko mbali na madhabahu ya Bwana, na Hekaluni,
anaukosa uwepo wa Mungu na uwepo wa Mungu unaibuka kuwa kiu yake kubwa, Yeye
kimsingi hakuwa analenga Baraka au uhitaji mwingine lakini yeye alikuwa na hamu
au kiu ya ushirika na Mungu yeye mwenyewe, kiu ya aina hii ni kiu yenye Baraka
kubwa sana kama watu watakuwa nayo
Mathayo 5:6 “Heri wenye njaa na kiu ya haki; Maana hao watashibishwa.”
Mwandishi alikuwa na kiu ya kusikia kutoka kwa Mungu, kiu ya neno la Mungu,
alikuwa na kiu ya kutaka kuabudu na kufurahia uwepo wake na ukaribu wake na
Mungu, Kumkosa Mungu kwake ilikuwa ni sawa na kuwa katika nyika au katika nchi ya
ukame, uhai wake ulikuwa unahitaji sana vitu hivi, alikuwa anatambua kuwa
ushirika kati yake na Mungu ndio chanzo cha Baraka nyinginezo zote, alitambua
kuwa ulinzi wake na usalama wake unategemeana sana na ukaribu wake na Mungu,
Maneno ya Mwandishi wa zaburi hii ni ya muhimu na ya msingi kwa kila mwanadamu
duniani, Unaishije bila kuabudu, unaishishe bila maombi, unaishije? Unategemea
nini na usalama wako ni nini Maisha yetu bila uwepo wa Mungu ni kujihatarisha
ni lazima tuwe na kiu na hamu na shauku ya mambo ya Mungu wetu, ziko nyakati
katika maisha tunaweza kukosa kabisa nafasi ya kuufurahia uwepo wa Mungu, Ayala
bila kunywa maji hata kama kuna chakula uwezo wake wa kuishi unapungua sana na
uwezo wake wa kujihami unapungua mno na mauti inakuwa karibu, uhai wake
unategemea sana maji na sisi nasi uhai wetu unamtegemea sana Mungu, mwandishi
wa zaburi alimtegemea sana Mungu sisi nasi hatuna budi kumtegemea sana Mungu na
kuona ya kuwa bila yeye sisi hatuwezi kuishi, Ayala hukimbia anakokimbia lakini
lazima atafute vijito vya maji ili maisha yaweze kuendelea, wewe na mimi
tunawezaje kuishi bila Mungu na bila kuwa na uhusiano naye? Ni lazima kuwa na
kiu kwa maswala ya Mungu, kiu ya kuabudu, kiu ya kujazwa na Roho wake
Mtakatifu, na kiu ya kumuabudu
Amosi 8:11-12 “Angalia, siku zinakuja,
asema Bwana MUNGU, ambazo nitaleta njaa katika nchi; si njaa ya kukosa chakula,
wala kiu ya kukosa maji, bali ya kukosa kuyasikia maneno ya Bwana.Nao
watatanga-tanga toka bahari hata bahari; na toka upande wa kaskazi hata upande
wa mashariki; watapiga mbio, wakienda huko na huko, kulitafuta neno la Bwana,
wasilione.”
Umuhimu wa kuwa na kiu kama Ayala.
Tunaona mwandishi akiomboleza kwa
sabahu alikuwa katika kipindi ha mateso na majaribu, na alikuwa na uhakika kuwa
Mungu ndiye msaada wake mkubwa, kwa hiyo kiu yake sio ya maji na chakula, ni
kiu ya uwepo wa Mungu kama zamani, ni kiu yanafasi ya kumuabudu Mungu,
inaonekana mwandishi aliwahi kuwa
Hekaluni na aliwahi pia kuongoza ibada, au kuongoza watu kuelekea ibadani
lakini sasa anakosa jambo hili muhimu, na anateseka, jambo hili linaibua kiu ya
kumuhitaji Mungu kwa wingi zaidi, Uhai wetu wa kiroho unategemea sana na
uhusiano wetu wa amani na Mungu, kila mwanadamu anahitaji hili, ni kiu hii ya
ndani ya kuhitaji ushirika na Mungu ndiyo inayotufanya tuwe na uwezo wa
kumtafuta Mungu, kiu hii husababishwa na Roho wa Mungu ndani
Yeremia 29:11-13 “Maana nayajua mawazo
ninayowawazia ninyi, asema Bwana, ni mawazo ya amani wala si ya mabaya, kuwapa
ninyi tumaini siku zenu za mwisho. Nanyi mtaniita, mtakwenda na kuniomba, nami
nitawasikiliza. Nanyi mtanitafuta na kuniona, mtakaponitafuta kwa moyo wenu
wote.”
Ayala anategemea sana Maji pia
sio kwaajili ya kunyumbulika kwa misuli yake lakini maji pia humfanya akue na
kuongezeka hatua kwa hatua, kiu ya uwepo wa Mungu hutusaidia katika ukuaji wetu
wa kiroho, Mtu aliyeokoka karibuni anaitwa mtoto mchanga wa kiroho, kama mtu
atakosa kiu ya neno la Mungu, na kiu ya ibada, na kiu ya kuutafuta uwepo wa
Mungu ni dhahiri kuwa ukuaji wake wa kiroho utaathiriwa anaweza kudumaa au kuwa
na miaka mingi katika wokovu lakini akiwa amebaki vile vile tu, kama kiu hii
itaondoka kwa kweli tunaweza kusema kuwa uhai nwako wa kiroho umeondoka! Kifo
cha kiroho kimetokea, Kama uzima wa kiroho uko ndani yako tamaa au kiu ya
kumtafuta Mungu itakuweko ndani yako nah ii ndio dalili ya uhai wako wa kiroho.
1 Petro 2:2 “Kama watoto wachanga
waliozaliwa sasa yatamanini maziwa ya akili yasiyoghoshiwa, ili kwa hayo mpate
kuukulia wokovu;”
Waebrania 5:11-14 “Ambaye tuna maneno mengi
ya kunena katika habari zake; na ni shida kuyaeleza kwa kuwa mmekuwa wavivu wa
kusikia. Kwa maana, iwapasapo kuwa waalimu, (maana wakati mwingi umepita),
mnahitaji kufundishwa na mtu mafundisho ya kwanza ya maneno ya Mungu; nanyi
mmekuwa mnahitaji maziwa wala si chakula kigumu.Kwa maana kila mtu atumiaye
maziwa hajui sana neno la haki, kwa kuwa ni mtoto mchanga. Lakini chakula
kigumu ni cha watu wazima, ambao akili zao, kwa kutumiwa, zimezoezwa kupambanua
mema na mabaya.”
Moja ya changamoto kubwa
inayolikabili Kanisa katika nyakati za leo, sio tu kukosa uamsho pekee lakini
pia kanisa limejawa na wakristo na hata watumishi waliodumaa kiroho, wako vile
vile miaka yote matendo ya mwilini yanaonekana wazi wazi, mafarakano na fitina
zinazonekana wazi wazi na hii ni dalili ya kuwa watu wamedumaa kiroho au
wamebaki katika hali ya uchanga ni kiu ya neno la Mungu na uwepo wake pekee
utakaotusaidia kukua kiroho siku hadi siku na kuondoka mwilini ona:-
1Wakorintho 3:1-3 “Lakini, ndugu zangu,
mimi sikuweza kusema nanyi kama na watu wenye tabia ya rohoni, bali kama na
watu wenye tabia ya mwilini, kama na watoto wachanga katika Kristo.
Naliwanywesha maziwa sikuwalisha chakula; kwa kuwa mlikuwa hamjakiweza. Naam,
hata sasa hamkiwezi,kwa maana hata sasa ninyi ni watu wa tabia ya mwilini.
Maana, ikiwa kwenu kuna husuda na fitina, je! Si watu wa tabia ya mwilini ninyi;
tena mnaenenda kwa jinsi ya kibinadamu?”
Ni kiu ya aina kama ile ya Ayala
ambayo kimsingi pia inaleta uamsho na uwepo wa Roho Mtakatifu unapohisi
kukaukiwa kiroho basi unayo kiu hii na Mungu ametoa wito kumpa maji ya uzima
kila mwenye kiu
Isaya 44:1-3 “Lakini sikia sasa, Ee Yakobo,
mtumishi wangu; na Israeli, niliyekuchagua; Bwana, aliyekufanya, na kukuumba
toka tumboni, yeye atakayekusaidia, asema hivi; Usiogope, Ee Yakobo, mtumishi
wangu; na wewe, Yeshuruni, niliyekuchagua. Kwa maana nitamimina maji juu yake
aliye na kiu, na vijito vya maji juu ya mahali pakavu; nitamwaga roho yangu juu
ya wazao wako, na baraka yangu juu yao utakaowazaa;”
Yohana 7:37-38 “Hata siku ya mwisho, siku
ile kubwa ya sikukuu, Yesu akasimama, akapaza sauti yake akisema, Mtu akiona
kiu, na aje kwangu anywe. Aniaminiye mimi, kama vile maandiko yalivyonena, mito
ya maji yaliyo hai itatoka ndani yake.”
Huduma za kiroho zinatolewa kwa
watu wenye kiu, kama mtu akipoteza kiu amepoteza uhai wa kiroho, Roho Mtakatifu
anatolewa kwa watu wenye kiu, kama huna kiu huwezi kupokea mito ya maji hai
inayoahidiwa na Neno la Mungu, Mungu anamtarajia kila mwanadamu awe na kiu hii,
sio wakati wa mapito na shida tu lakini kila siku kama tunavyohitaji maji
katika maisha yetu tunamuhitaji na Mungu pia, Mtu wa rohoni aliye hai ni yule
mwenye kiu, kiu yake inamlazimisha kufika katika ibada za mafundisho katikati
ya wiki, na siku za ibada kuu kila jumapili, na kumtafuta Mungu sisi wenyewe
binafsi,tukiwa na kiu hii Mungu hutujalia neema na utoshelevu wa kiroho, Ayala
huyatafuta maji kwa gharama yoyote hata kama yako mbali anajua uhai wake
umeungamanishwa na maji, sisi nasi tunapaswa kumtafuta Mungu kwa bidii kama Ayala
ayatafutavyo maji ya mto, Mwandishi ameonyesha wazi kuwa kama Ayala asivyoweza kustahimili
maisha bila maji, sisi nasi hatuwezi kustahimili maisha bila uwepo wa Mungu, ni
kiu yetu ndiyo inatayotupeleka katika vyanzo ma maji ya uzima na kutupa wakati
wa kuburudishwa na Roho Mtakatifu jambo litakalofungua baraka kubwa za kiroho
katika maisha yetu ya kila siku na kuchochea ukuaji wa kiroho na ukomavu wake!
“Nafsi yangu yakutamani, Nafsi
yangu yaona kiu, Kama Ayala atafutavyo maji ya mto, Bwana nafsi yangu
yakutamani, Nijaze Roho Mtakatifu, niweke karibu na wewe, Kama Ayala atafutavyo
maji ya mto Bwana nafsi yangu yakutamani”
Na. Rev. Innocent Samuel Kamote
Mkuu wa wajenzi mwenye Hekima.

.jpg)

