Jumanne, 12 Mei 2020

Mtego wa shughuli Nyingi!

1Petro 4:15 “Maana mtu wa kwenu asiteswe kama mwuaji, au mwivi, au mtenda mabaya, au kama mtu ajishughulishaye na mambo ya watu wengine.  

Utangulizi:
 Ni muhimu kufahamu kwamba ili mtu wa Mungu aweze kuwa imara kiroho anahitaji muda mwingi wa kukaa katika uwepo wa Mungu, kuomba, kujisomea neno na kutafakari na kuimba na kujizatiti kiroho kuliko tunavyoweza kufikiri, maandalizi yetu ya kiroho binafsi ni muhimu kwa ushindi dhidi ya ibilisi kuliko hata huduma, Mojawapo ya mbinu kubwa sana anayoitumia ibilisi ili kuwamaliza watu wengi kiroho na hatimaye ili aweze kuwaangusha ni kuwaingiza katika MTEGO WA SHUGHULI NYINGI kwa msingi huo ni muhimu kwetu kuijua mbinu hii ili shetani asipate kutushinda kwa kutokuzijua mbinu zake angalia  2Wakoritho 2:11 “Shetani asije akapata kutushinda; kwa maana hatukosi kuzijua fikira zake Biblia ya kiingereza inatumia maneno “Let Satan should get advantege of us – yaani asije akapata faida, akapata kitu kwetu, akafaidika, kwa mbinu “Fikra” zenye hila zenye kuumiza zenye ujanja cunning strategies mbinu anazitumia adui ili aweze kutushinda, Biblia inatutahadharisha kuwa wajuzi na wajanja katika mbinu za ibilisi ili asitunase, moja ya mbinu hii ni mtego wa shughuli nyingi!
Shetani anajua nguvu zako na uweza wako ulio nao, anajua wazi kuwa asili ya nguvu zako iko katika chanzo cha ngubu za Roho Mtakatifu unachokitegemea, ambacho kimeungwa katika kujityoa kwako binafsi kwa Mungu self devotional kwa msingi huo hataki na wala hatakubali upate nafasi ya kurudi magotini na katika kulisoma neno la Mungu na badala yake atakupa kitu mbadala ili akutumie kwenye hilo na baada ya muda flani aje na mbinu zilezile za kukuangusha ukiwa mtupu kabisa, mtego huu na mbinu hii anayoitumia shetani ni Mtego wa shughuli Nyingi.
Ni muhimu kufahamu kuwa unaweza kuwa unampenda Mungu sana na unapenda sana uwe na Muda wa kuomba na kububujika katika uwepo wa Mungu, unapenda upate nafasi ya kufunga na kuomba na kutafakari neno na kuhudhuria ibada na kufanya mambo yote yatakayokuweka karibu na Mungu na kuna uwezekano kabisa umekomaa kiroho na umefikia ngazi ambayo hakuna jaribu jipya litakuja kwako usilibaini, Shetani akiisha kufahamu hilo hatakuwa na Majaribu ambayo anajua kuwa utashituka kwa haraka bali atakuja na Mtego wa shughuli nyingi, kwa mtego huu atakutumia kwa muda mrefu uwe unashughulika na mambi mengi sana ambayo yanaweza kuwa kama ya kiroho hivi lakini baada ya Muda utagundua kuwa umepungukiwa sana na uwepo wa Mungu na katika wakati huu anaweza kukusambaratisha atakavyo akihakikisha kuwa hauna na wala haupati nguu ya kuinuka tena!  
Binafsi Kuna jambo nimekuwa nikimuomba Mungu sana, kuhusu maisha yangu katika siku za karibuni ili kwamba Mungu aweze kuingilia kati na kunisaidia, nampenda sana Mungu, napenda sana neno lake na napenda sana kuomba na pia kuandaa jumbe za neno la Mungu kwa kusudi la kuwasaidia watu wake, napenda kukaa uweponi mwake,  hiyo ni kazi yangu, ni wajibu wangu ndio kazi niliyoitiwa, nimeitwa kuujenga mwili wa Kristo na hili nalifanya kwa uaminifu, Lakini nahisi kuna kitu kimepungua kwangu, nahisi kiu ya kumuhitaji Mungu, nafanya kazi yake lakini nahisi nimemmisi Mungu, sio yeye tu nimemisi pia baadhi ya watu, ndugu zangu jamaa zangu na hata marafiki zangu nahisi kama kuna jambo ninapoteza sio kiroho bali na hata kimwili, kwa sababu hata ratiba ya kula haiko sawasawa nimekuwa na shughuli nyingi mno mno nikiwa natafakari hilo siku moja nikaelewa kuwa ni mtego wa Ibilisi!
Fikiaria kama unaweza kuwa na shughuli nyingi, kiasi cha kutokuwa na Muda na marafiki, jamaa, familia, mkeo, wanao, na hata muda wa kula au ahata kufanya mazoezi na unarejea nyumbani ukiwa umechoka mno, hata kula kwenyewe unaona uvivu! Kumbuka shughuli ulizokuwqa ukizifanya sio dhambi hata kidogo ni shughuli zilizoko katikati yako na huduma yako, kwa hiyo ni kama za huduma yako, wale watu waliofikia ngazi ya kuwa viongozi, Maasskofu, waangalizi, mitume na manabii watakubaliana nami katika hili kuwa kadiri unavyokuwa na majukumu haya makubwa na shughuli zionaongezeaka mno ni shughuli za kati kati katika ya uwepo wa Mungu na uwepo wa dunia hapa ndipo shetani anapokuweka kwa kusudi la kukuingiza katika mtego huu ninaouzungumzia shetani anaogopa sana akuachie mtu kama wewe ukae katika uwepo wa Mungu anajua utampa shida sana angalia mistari ifuatayo:-

Luka 4:1-2 “Na Yesu, hali amejaa Roho Mtakatifu, alirudi kutoka Yordani, akaongozwa na Roho muda wa siku arobaini nyikani, akijaribiwa na Ibilisi. Na siku hizo alikuwa hali kitu; hata zilipotimia, aliona njaa

Luka 4:14-15 “Yesu akarudi kwa nguvu za Roho, akenda Galilaya; habari zake zikaenea katika nchi zote za kandokando. Naye alikuwa akifundisha katika masinagogi yao, akitukuzwa na watu wote.”

Katika maandiko hayo hapo juu Yesu alikaa katika uwepo wa Mungu kwa muda wa kutosha alikuwa anafunga na kuomba alishinda majaribu yote makubwa ya ibilisi, na sasa anaingia katika jamii akiwa na NGUVU ZA ROHO nguvu hizi ndio zinazomfanya Yesu anakuwa maarufu kil a mahali habari zake zinaenea kila sehemu na watu wote wanamsifu na kumtukuza, Kukaa katika kuutafuta uwepo wa Mungu ni jambo la muhimu na lenye kumuogopesha sana shetani kuliko jambo lolote lile shetania anajua ni vigumu kumshinda mtu anayekaa katika uwepo wa Mungu lakini ni rahisi sana kumpata mtu kwa kumfanya ashighulike na mambo ya wengine kuliko kushughulika na yeye binafsi

Jambo hili hunitokea na mimi bila kupenda unakuwa busy unakuwa na shughuli nyingi tu zenye kuchosha  nikitafakari wakati mwingine naingia shaka kama yanafanana na kile Mungu ameniitia au nimeingia katika metgo wa ibilisi? Siku moja nikiwa nimechoka majira ya saa tatu usiku nikiwa nimevaa suti niliyoivaa tangu asubuhi, na nikiwa sijachukua mazoezi wala kuoga nikiwa nawasubiri watu fulani ambao nilikuwa na kikao nao tangu asubuhi mpaka saa sita nikaenda kunywa chai ya mchana, kisha wao wakenda mjini na kuniahidi watarejea na hivyo nikawa nawasubiri warejee mpaka ilipofika saa tatu usiku waliniahidi wanakuja nikaendelea kusubiri sikubadilisha nguo sikutaka kuondoa nguo nzito mwilini mwangu nawasubiri watu wa Mungu niwahudumie, nilipompigia simu mmoja akaniambia ndio yuko mezani anakula ameshindwa kurudi kha mimi nilikuwa sijaweza kufanya jambo lolote namshubiri yeye, nilimweleza mke wangu naye akaniambia omba ili kwamba roho ya Masumbufu ikuachie unakuwa busy sana lakini ni ubize ambao ni kama unakutesa wewe, ratiba za kula hazikai vizuri, ratiba za mazoezi huzifuati sawasawa, kukaa na familia na hata muda wako wa kuandaa neno la Mungu kaa sawa alinieleza mke wangu!

Nikaomba na kumuuliza Mungu mbona maswala yasiyo ya muhimu lakini yanayoonekana kama ni ya muhimu sana yananiandama maisha yangu  naona nashughulika nayo kuliko yale niyapendayo kuyatenda? Ndipo Roho Mtakatifu akaniambia “UMEINGIA KATIKA MTEGO WA SHUGHULI NYINGI”

Nilifikiri ninamtumikia Mungu na ninafanya kazi zake sasa nimeingiaje kwenye mtego washughuli nyingi? Nilikuwa najiuliza mbona kazi zimeongezeka sana nyingine njema ni za kazini, na taasisi yetu ni ya kimungu tunamtumikia Mungu sasa nimeingiaje kwenye mtego wa shughuli nyingi? Ni Mungu ndiye aliyeniita nilidhani kuwa wakati huu nimekuwa na shughuli nyingi kwa sababu nimekuwa mtu mzima kwa hiyo majukumu yananipeleka nisikokutaka nilijipa moyo kwa neno la Mungu Yesu alimwambia Petro ulipokuwa kijana ulikwenda kokote ulikotaka wewe utakapokuwa mtu mzima mtu mwingine atakufunga na kukupeleka usikotaka, Yesu alikuwa anaongelea juu ya mauti ya Petro katika Yohana 21:18 “Akasema, Amin, amin, nakuambia, Wakati ulipokuwa kijana, ulikuwa ukijifunga mwenyewe na kwenda utakako; lakini utakapokuwa mzee, utainyosha mikono yako, na mwingine atakufunga na kukuchukua usikotaka.” Tafasiri ya Maneno haya ya Yesu ipo katika mstari wa 19 Yesu alitabiri namna Patro atakavyokufa akimtukuza Yesu, Mimi niliutumia mstari wa 18 pekee kukubali tu ukweli kuwa ukiwa kijana unakuwa na uhuru mkubwa wa kujifanyia lolote ulipendalo nafasi inakuwa nyingi mno na  unaweza kwenda kokote utakako ukiisha kuwa mtu mzima na mwenye majukumu shughuli zinakufunga kiasi ambacho huwezi kufanya utakalo, bali majukumu yanakulazimisha uyafanye nilitumia maandiko haya kujipa moyo kuwa huenda ndio mambo yalivyo lakini Roho Mtakatifu alisisitiza tu “UMEINGIA KATIKA MTEGO WA SHUGHULI NYINGI” UMEINGIA KATIKA MTEGO WA SHUGHULI NYINGI?

Sasa niliamua kuwa mpole na kumsikiliza Roho Mtakatifu, lakini pia safari hii nilimsikiliza mke wangu, ni nadra sana kwangu kusikiliza mwanamke narudia tena ni nadra sana kwangu kumsikiliza mwanamke hii niachie mwenyewe labda yatokana na athari zangu za kimaandiko na kimaisha huwa simsikilizi mwanamke  aaa huwa namsikiliza sana lakini kwa vile niko  na shughuli nyingi (busy) na huwa anazungumza habari nyingine za kwenye mitandao ya kujamii huwa nahesabu kama mtu anayeweza kunipotezea Muda lakini safari hii alichoniambia “omba ili kwamba roho ya Masumbufu ikuachie u nakuwa busy sana lakini ni ubize ambao ni kama unakutesa wewe,” akili ilinijia kuwa nachoka sana na kufadhaika sana kwa shughuli nizifanyazo kila siku nikihangaikia watu na taasisi  nimekuwa  na shughuli nyingi kweli kweli busy mno hakuna wakati wakupumzika,  shughuli zenyewe ukizitafakari sio dhambi ila ziko katikati ya shughuli za kimungu ni shughuli za kanisa kabisa lakini hazikupi nafasi ya kuukaribia uwepo wa Mungu hizi ndio zinaitwa Mtego wa shughuli nyingi, Mtego huu ndio Ibilisi anautumia kulikamata kanisa la leo, chunguza kwa undani makanisani kila idara ina shughuli, kanisa lina shughuli wachungaji wanashughuli, kuna shughuli za VIJANA, Kuna shughuli za WAMAMA, kuna shughuli za WABABA, kuna shughuli za UJENZI, kuna shughuli za UINJILISTI, kuna shughuli za Vikao vywa WACHUNGAJI, Kuna shughuli za WAANGALIZI, kuna shughuli za MAASKOFU kuna shughuli za UMOJA WA MAKANISA, kuna shughuli, Kuna mipango kadhaa ya maswala kadhaa, kuna shughuli nyingi mno, siku moja nilifika kwenye kituo Fulani cha Polisi kwenye shughuli nikamuona rafiki yangu mmoja ASKOFU wa kanisa Fulani aliwa pale POLISI mimi nilikwenda kutoa taarifa ya mhasibu wetu alikuwa amechukua fedha nyingi za taasisi yetu zilizotakiwa kwenda TRA na tulipokuwa tunambana azirudishe akawa hato maelezo yaliyonyooka kwa hiyo nilimpeleka POLISI na ilinipasa kufika hapo kuandikisha maelezo sikuwa na nania ya kumfunga lakini nilitaka pesa zirudi tu zilikuwa milioni 16, sikuwahi kufikiri kuwa nitafika Polisi hata siku moja, Nilishangaa kumuona Askofu yuko pale, Nilimuuliza Mchungaji Vipi mbona uko hapa akaniambia kuna Mchungaji wangu yuko Ndani amefungwa nimekuja kumletea chakula tulikaa sana pale kituoni wakati huu somo hili lilikuwa ndio linafunuliwa kwangu upesi nikajisemea Moyoni ni “ULE MTEGO WA SHUGHULI NYINGI” ulimwengu umekuwa wa shughuli nyingi, ninasimamia shule ya Seminary mahali ambapo injili inahubiriwa wanafunzi wetu ni wa kiume tu baadhi ya wanafunzi watatu walijihusisha na dhambi ya USHOGA tukawafukuza, wazazi wao wakapingana nasi vikali, wakitaka vijana wao warudishwe shuleni, Afisa Elimu wilaya na Mkoa pia walisimama na wazazi ili kuwatetea warejee shuleni, Msimamo wetu ni kuwa hatuwezi kuwarudhisha shuleni wanafunzi waliokiuka maswala ya uadilifu kwa kiwango kama hiki, ilikuwa shughuli kubwa sana, vikaoa kadhaa vilikaliwa, vikao vya Kamati ya nidhamu, vikao vya walimu, vikao vya bodi ya shule, vikaoa na wazazi vikao na maafisa Elimu, vikaoa na watu wa usalama wa taifa  ilichukua miezi mitatu kuumaliza mgogoro huo wa kuvutana sisi HAWARUDI maafisa Elimu wanasema WATARUDI lilikuwa jambo la kushangaza viongozi wakubwa wanaotakiwa kusimamia uadilifu katika maswala ya Elimu wakitetea ujinga na uchafu, tena wakisema haifai Mchungaji kuwa mkuu wa shule? Nilikuwa naumia moyoni nilitamani Mungu afanye kitu flani na Mungu alifanya lakini mapambano hayo dhidi ya uovu yalichukua miezi mitatu kumalizika na kumbuka maafisa Elimu wote walikuwa wakristo na wazazi wa watoto walioshiriki uovu ule walikuwa wakristo kwa nini shetani alikuwa akitusumbua hivi dunia imeharibika ibilisi alikuwa anataka tuwe na shughuli nyingi tujiumize na kujichosha kwa jambo rahisi la walioshiriki vitendo viovu kinyume na sheria za shule na imani yetu na neno la Mungu walitakiwa kuondoka mara moja lakini tulitumia miezi mitatu kuvutana shetani alitaka kuleta usumbufu na kutuingiza katika mtego wa shughuli nyingi. Sasa basi ni muhimu kujihoji basi mtego wa shughuli nyingi ni nini?
Maana ya Mtego wa shughuli Nyingi.
Nilijiuliza kwanza huu mtego wa shughuli nyingi ni upi? Katika moja ya mafunzo ya awali sana ya wokovu tulijifunza kuhusu kuwa na shughuli nyingi kunavyozuia ukuaji wa mtu kiroho hasa kupitia mfano wa Mpanzi ambapo zile mbegu zilizoangukia katika miiba humaanisha watu wanaolipokea neno la Mungu, lakini kwa sababu ya kusongwa na shughuli za ulimwengu wanashindwa kukua vizuri na hatimaye kushindwa kuzaa matunda! tujikumbushe maana za mfano ule


Mathayo 13:18-23 “Basi ninyi sikilizeni mfano wa mpanzi.Kila mtu alisikiapo neno la ufalme asielewe nalo, huja yule mwovu, akalinyakua lililopandwa moyoni mwake. Huyo ndiye aliyepandwa karibu na njia.  Naye aliyepandwa penye miamba, huyo ndiye alisikiaye lile neno, akalipokea mara kwa furaha; lakini hana mizizi ndani yake, bali hudumu kwa muda; ikitukia dhiki au udhia kwa ajili ya lile neno, mara huchukizwa. Naye aliyepandwa penye miiba, huyo ndiye alisikiaye lile neno; na shughuli za dunia, na udanganyifu wa mali hulisonga lile neno; likawa halizai. Naye aliyepandwa penye udongo mzuri, huyo ndiye alisikiaye lile neno, na kuelewa nalo; yeye ndiye azaaye matunda, huyu mia, na huyu sitini, na huyu thelathini.”


Nilitafakari sana kifungu hiki cha maandiko kwamba je inawezekana kwamba nimegeuka kuwa kundi la wale waliopandwa kwenye miiba? Ambao shughuli za dunia na udanganyifu wa mali hulisonga neno lisikue?au lisizae, sitaki kujihesabia haki sitafuti vitu vya dunia nimeridhika Mungu amenipa kila kitu ambacho mwanadamu wa kawaida anatakiwa kuwa nacho sitaki mambo makubwa kwa hiyo udanganyifu wa mali hauwezi kunisumbua lakini naweza kukiri kuwa shughuli za dunia zimenifunga, shughuli za dunia ni nyingi na sio lazima ziwe dhambi, lakini ni kazi za kawaida lakini hili silo lile ambalo Roho Mtakatifu alimaanisha.


Kwa hiyo nilitafakari kifungu kingine Katika wimbo uliobora 1:6 “Msinichunguze kwa kuwa ni mweusi-mweusi, Kwa sababu jua limeniunguza. Wana wa mamangu walinikasirikia, Waliniweka niwe mlinzi wa mashamba ya mizabibu; Bali shamba langu mwenyewe sikulilinda.“


Kifungu hiki pia sio tatizo kubwa sana huyu ni mtu ameajiriwa na au amefanywa mtumwa maisha yake yamemlazimisha kuwa mtumishi wa wengine kiasi ambacho ameshindwa kutimiza wajibu wa kuangalia mambo muhimu yanayiomuhusu yaani shamba lake mwenyewe la mizabibu, huu sio mtego wqa shughuli nyingi  ni mazingira flani tu ya kuajiriwa na kutokufanya maswala yako mwenyewe, hili halikuwa lile ambalo Roho Mtakatifu alikuwa analikemea kwangu “UMEINGIA KATIKA MTEGO WA SHUGHULI NYINGI”
Kwa hiyo nilitafakari kifungu kingine tena kuhusu siku ile Yesu alipomtembela Martha na Mariamu ona 


Luka 10:38- 42 ”Ikawa katika kuenenda kwao aliingia katika kijiji kimoja; mwanamke mmoja jina lake Martha akamkaribisha nyumbani kwake. Naye alikuwa na umbu lake aitwaye Mariamu, aliyeketi miguuni pake Yesu, akasikiliza maneno yake. Lakini Martha alikuwa akihangaika kwa utumishi mwingi; akamwendea, akasema, Bwana, huoni vibaya hivyo ndugu yangu alivyoniacha nitumike peke yangu? Basi mwambie anisaidie. Bwana akajibu akamwambia, Martha, Martha, unasumbuka na kufadhaika kwa ajili ya vitu vingi; lakini kinatakiwa kitu kimoja tu; na Mariamu amelichagua fungu lililo jema, ambalo hataondolewa.”


Hichi alichokisema Yesu kwa Martha kilikuwa ni cha Muhimu sana angeweza kuketi kama Mariam na kumsikiliza Yesu ambaye anauwezo hata wa kushusha chakula kutoka mbinguni, Yeye alikuwa akisumbuka kwaajilya kumpikia Yesu hakikuwa tatizo kama Martha  angepika na kuleta chakula  kwa Yesu angekula yeye ni mwanadamu kwa wakati ule angekula lakini tatizo la Martha alinung’unika na kushitaki kuhusu Mariamu Hivyo Yesu alitaka kuonyesha ubora wa Mariamu kwa upande mwingine kumsikiliza Yesu na kukaa minguuni pake ni shughuli muhimu sana, Kuliko alichokuwa anakifanya Martha,  Martha alikuwa  na shughuli nyingi (busy) lakini hili halikuwa tatizo isipokuwa kama tu amenung’unika lakini shughuli yake ilikuwa ni sahihi kimila na kitamaduni kushughulika kwaajili ya Yesu  aliyekuwa mgeni wao haikuwa tatizo kama tutakuwa na shughuli nyingi bila kuwanu;gunikia wengine sio tatizo, mimi ninashughulika kwaajili ya Yesu na sitaki kumlaumu Mtu lakini hili sio lile ambalo Roho Mtakatifi analikemea kwetu Mungu anatuonya na kutukemea kuhusu hili  “UMEINGIA KATIKA MTEGO WA SHUGHULI NYINGI”


Andiko la msingi hasa linasema hivi 1Petro 4:15 “Maana mtu wa kwenu asiteswe kama mwuaji, au mwivi, au mtenda mabaya, au KAMA MTU AJISHUGHULISHAYE NA MAMBO YA WATU WENGINE.


Nitalinukuu andiko hili pia kwa lugha ya kiingereza uweze kuliona vizuri kile kinachomaanishwa hapa 1Peter 4:15 “If you suffer, It should not be as a murderer or thief or any other kind of criminal or EVEN AS A MEDDLER” Neno Meddler – maana yake mwenye kujishughulisha na mambo ya watu katika njia isiyo sahihi, au yenye kuingiliana na shughuli muhimu za kazi, au kujishughulisha ma maswala yasiyopaswa au yasiyotakiwa toleo lingine la kiingereza linatumia neno “Busybody” mtu anayeteseka kwa kujishughulisha na mambo ya wengine yanayoonekana kama mambo yake  au ya Mungu lakini sio ya Mungu KJV inasema hivi  1Peter 4:15But let none of you suffer as a murderer, or as a thief, or as an evildoer, or as a busybody in other men's matters.”



 

Mtu aliyeingia katika mtego wa shughuli nyingi ni mtu anayejishughulisha na maisha ya wengine lakini mtego huu ni mtego wa dhambi isiyokusudiwa, hili ni tatizo kubwa sana unajishughulisha na mambo ambayo sio kazi ya wito wako Mungu aliokuitia na hili pekee ni tatizo tosha na mbaya zaidi mtu mwenye kujishughulisha na mambo ya wengine ana muda mchache au hana muda kabisa wa kushughulikia mambo yake, hawafanyi dhambi lakini wakati wote hufukiri kuhusu wengine hawana muda wa kutubu husaidia wengine kutubu, hawana muda wa kusoma neno husaidia wengine kuelewa neno, hawana Muda kuomba huhamasisha watu kuomba, hawana muda hata wa kula huhudumia watu walioshiba huku yeye akiwa na njaa, hutatua matatizo ya wengine huku yake hakuna anayeyajali kwa ujumla wanapoteza lengo na hawana muda hata wa kujitathimini, wanaweza kunyoosha kidole kwa wengine huku vitatu vikiwarejea wenyewe ikiwa ni ishara ya Mungu Baba Mwana na Roho Mtakatifu wakitusihi kujiangalia wenyewe zaidi kujitathimini na kujilinda na kujihami



 

Huu ni mtego wa Ibilisi anatufanya tupeleke mawazo yetu kwenye kitu vitu ambavyo havitaweza kubadilika ili kwamba tusiweke mawazo yetu katika mabadiliko yetu wenyewe, ni kwaajili ya haya Shetani anataka tuangalie mambo ya wengine ambao ni vigumu kuwabadilisha ili kwamba tusijiangalie wenyewe ambao tunauwezo wa kubadilika kwa haraka kumbuka mtu aliyebadilika yeye mwenyewe ndio mwenye uwezo mkubwa zaidi wa kuwabadilisha wengine, shetani haogopi mtu anayeshughulikia mambo ya wengine bali anaogopeshwa zaidi na mtu anayetumia muda mwingi kwa mabadiliko yake mwenyewe



 

Kwa hiyo utaweza kuona kuwa na shughuli nyingi sio sifa bali ni wazi kuwa ni mtego wa Ibilisi, kukaa kwetu katika uwepo wa Mungu na kubadilika kwetu ndio kwa muhimu zaidi na kunakoweza kubadilisha wengine kuliko shughuli zetu za kushughulika katika kubadilisha mambo!

 



Shetani amefanikiwa kwa kiwango kikubwa sana kulipa kanisa kuwa na shughuli, makanisa mengi  leo yana mipango na shughuli na watumishi wengi wa Mungu leo wanashughulikia mipango na shughuli, vijana wako kwenye mipango na shughuli, wamama wako kwenye mipango na shughuli, wababa wako kwenye mipango na shughuli, waangalizi wa makanisa wako kwenye mipango na shughuli, maaskofu na viongozi wako kwenye mipango na shughuli, Muda mwingi unaotumika ni wa vikao vya mipango na shughuli wajkati mwingine vikao vya mipango na shughuli ndio huwa vinakuwa virefu kuliko hata ibada yenyewe leo washirika wanakwenda katika ibada lakini wakiwa wamejaa mawazo ya mipango na shughuli, penginepo watatakiwa kutoa taarifa ya mipango na shughuli sasa haya nyanapozidi kuliko yale tutakayoyatolea Hesabu atakapokuja mwana wa Adamu ndio yanaitwa mtego wa Ibilisi na mtego huu una madhara yake angalia kisa kifuatacho:-



 

Baba Mtakatifu Gregory the great (Pichani hapo Juu) wakati wa mwisho wa huduma yake ya kichungaji alikuwa akitafakari kuhusu swala zima na kujishughulisha na mambo ya wengine yeye alitumia mfano wa stori ya Dina katika Biblia hakutumia neno Mtego wa shughuli nyingi bali alifananaisha na kile kinachomtokea mtu aliyenaswa na mtego wa shughuli nyingi, alisema kwanza shetani hutoa mawazo yenye ushawishi kwa mtu ili kumuhakikishia ulinzi na usalama wa uongo kwa kusudi la kumbomoa mtu huyo polepole na mfano huu ni sawa na yake yaliyomtokea Dina.
Mwanzo 34:1-3Basi Dina, binti Lea, ambaye Lea alimzalia Yakobo, akatoka kuwaona binti za nchi. Shekemu, mwana wa Hamori, Mhivi, mkuu wa nchi, akamwona akamtwaa, akalala naye, akambikiri. Moyo wake ukaambatana na Dina binti Yakobo, akampenda huyu msichana, akasema na huyu msichana kwa maneno mazuri.” 


Dina alitoka kwenda kuwaona mabinti wa nchi, kila mara mtu anapoacha kuifikiri nafsi yake na kuanza kujishughulisha na wengine Shekemu mtawala wa dunia ataiwinda nafsi hiyo na kuibikiri au kuitia unajisi, shetani nwakati wote huitia unajisi nafsi ya mtu inayojishughulisha na mambo ya nje wakati mwingine bila yeye kujua na shetani atazungumza na wewe kwa maneno mazuri, kwa sababu shetani anatufikiri sisi kuwa watu wenye kufaa kwake  shetani wakati wote atatupa tumaini la uongo lakini hatima yake ni kututia unajisi tu, habari ya Dina ni sawa na mtu anayeingizwa taabuni na shetani, Shetani ataendelea kuzungumza vizuri na mtu anayejishughulisha na mambo ya wengine ili aweze kumnasa katika mtego wake (Binti Bikira wakati wote huwakilisha Kanisa, Binti za nchi huwakilisha wana wa dunia hii na Mfalme wao huwakilisha Mungu wa dunia hii yaani Shetani)


Inawezekana tukawa hatufanyi dhambi, lakini tukanaswa katika mtego wa shughuli nyingi, tukionana  na kukutana na watu wa dunia hii wenye dhambi na wakatutia unajisi kwaajili ya kushughulika nao, tunapaswa kulinda nafsi zetu zisiondoke katika ushirika na Mungu, shetani anataka tuwe na shughuli nyingi (busy) na shughuli za dunia tushughulike na wenye dhambi na kujisahau taratibu, anataka atunase duniani taratibu tutapungua katika kusimamia neno la Mungu, tutapungua katika kuomba, tutapungua katika kuhudumu, kuhudhuria ibada, kutenda mema kuona wagonjwa, kuhudumia yatima, kujenga ushirika, kujenga umoja, kukuza familia kuimarisha ndoa, kukuza ndugu kuonyesha kuwajali baba na mama na washirika weengine, tutakuwa na shughuli nyingi kiasi cha kushindwa kusimamia watoto wetu na malezi yao na masomo yao, tutakuwa na shughuli mno mpaka tunachoka na kushindwa kuona umuhimu wa wa kuwa karibu na Mungu, Kumbuka Dunia haibadilishwi na watu wanaobadilisha wengine bali inaweza kubadilishwa na watu waliobadilika wao wenyewe kwanza, “unapojaribu kubadilisha wengine utayeyuka mwenyewe kama sabuni” tunaposhughulika na wengine tunaweza kuingia vilevile katika mtego wa kujilinganisha nao na kuona aaa mimi sio mbaya sana ukilinganisha na hawa na shetani anaweza kutunasa kijanja sana na kuzungumza lugha nzuri na sisi bila sisi kuelewa kuwa tumeingia katika mtego wa shughuli nyingi,


Mtu aliyechoka kwa shughuli nyingi anapoteza uwezo wa kuona mambo ya Msingi ya kiroho, Kutokana na kuchoshwa kwa shughuli nyingi tunapoteza kujitambua kuwa sisi ni nani kwa Mungu, tunaweza kujikuta tunapuuzima mambo ya msingi kwa sababu tu shughuli nyingi zimetuzinga, mtu mwenye utulivu wa nafsi anaweza kuina kwa jicho lingine na kuyapima mambo kwa uzito unaiostahiki kuliko mtu aliyechoka, Shetani anajua nguvu zako na uwezo wako wa kiroho anajua kuwa unatambua mbinu zake zote kwa kiwango kikubwa anajua uzoefu wako hivyo hawezi kukupata tena vilabuni, hawezi kukupata tena kwa zinaa, hawezi kukupata tena kwa majaribu na mateso lakini anajua akikuacha ufanye shughuli nyingi sana utachoka na kwa urahisi sana atakubembeleza wakati umechoka na kukuchukulia kitu chako cha thamani kile ambacho Mungu amekupa ni wakati gani Esau aliuza urithi wake wa Mzaliwa wa Kwanza ni wakati amechoka na uwezo wa kufikiri umepungua 

Mwanzo 25:29-34 “Yakobo akapika chakula cha dengu. Esau akaja kutoka nyikani, naye alikuwa amechoka sana. Esau akamwambia Yakobo, Tafadhali, unipe hicho chakula chekundu nile, kwa kuwa ninazimia mimi. Kwa hiyo walimwita jina lake Edomu.Yakobo akamwambia, Kwanza niuzie leo haki yako ya mzaliwa wa kwanza. Esau akasema, Tazama, mimi ni karibu kufa, itanifaa nini haki hii ya uzazi? Yakobo akamwambia, Uniapie kwanza. Naye akamwapia, akamwuzia Yakobo haki yake ya mzaliwa wa kwanza. Yakobo akampa Esau mkate na chakula cha dengu, naye akala, akanywa, kisha akaondoka, akaenda zake. Hivyo Esau akaidharau haki yake ya mzaliwa wa kwanza.”


Jinsi ya kujitoa katika Mtego wa shughuli nyingi!.


Ni lazima tuchukizwe na hali ya kudhalilishwa na kubakwa na na kunajisiwa na ibilisi na kukataa kumuacha azungumze nasi lugha nzuri ya kutupendezesha, Lazima uamke na kujipima na siku za mwanzoni mwa wokovu wako tulipokuwa tunaomba sana na kusoma neno la Mungu sana mambo yalirahisishwa na wala hatukuwa na shughuli nyingi, sasa angalia tuna shughuli nyingi lakini je tunaomba kama zamani je haujihisi kupungukiwa na kitu? Sasa basi tufanye nini lazima tukubali kujipima sawa na neno la Mungu!


Ni lazima tujishughulishe sana katika kuomba ili Mungu atuepushe na mtego wa shughuli nyingi na kuhakikisha kuwa hatukubali kuwa washirika wa shughuli  nyingi na kumpa Ibilisi nafasi, jambo moja la msingi la kukumbuka ni kuwa mtu mwenye shughuli nyingi ni mawindo rahisi sana ya ibilisi, kwa kuwa tunaangalia sana mambo ya wengine kiasi cha kusahau kuangalia mambo yako mwenyewe, ni rahisi kunajisiwa na kuingia katika taabu kwa sababu ya kushughulika na mambo ya wengine, unaweza tu kusahaulishwa na ule mpango wa ibilisi wa kukulinganisha kuwa hata hivyo mimi sio mbaya sana ukilinganisha na wengine, unaweza tu kujifikiri kuwa wewe ni bora sana ukijilinganisha na wengine kumbuka kuwa kiwango cha ubora wetu si watu wengine bali ni Yesu Kristo yeye ndio kielelezo chetu na kiwango cha ubora wetu na ni kupitia neema na rehema tunaweza kufikia kiwango chake tatizo kubwa la watu walioingia katika mtego wa shughuli nyingi ni kuwa wanajishughulisha sana na mambo ya wengine na wanasahau kujihukumu wenyewe kwa msingi huo basi ni muhimu kwanza


1.       1Wakoritho 11:31 “Lakini kama tungejipambanua nafsi zetu, tusingehukumiwa.”  Kila mtu aliyeokoka anapaswa kujipima mwenyewe na kujiangalia mara kwa mara kwamba yuko katika kiwango gani cha kumpenda Mungu na kuacha shughuli nyingi na kujitoa zaidia katika dua na sala na maombi na kulia sana machozi


2.       Tunapaswa kujilinda na kujihami na sifa tunapofanya kazi ya Mungu wakati mwingine watu watatusifu na wenye mahitaji yao wengi watatujia tutajikuta tunawahudumia sana wao na kusahau kuwa nguvu za kuwahudumia hazitokani na nafsi zetu tuuige mfano wa Yesu ambaye mara kadhaa alijitenga na umati wa watu waliokuja kwa nia njema ili awahudumie lakini yeye alikumbuka kwenda kuomba angalia Luka 5:15-16Lakini habari zake zikazidi kuenea, wakakutanika makutano mengi wamsikilize na kuponywa magonjwa yao. Lakini yeye alikuwa akijiepua, akaenda mahali pasipokuwa na watu, akaomba.” Leo hii wako watu wanafanya huduma na kushinda wakishughulika na watu kuanzia asubuhi mpaka jioni wanasahahu kuwa ni mtego wa shughuli nyingi Yesu alikumbuka mara kwa mara kujiepusha na kwenda kuomba


3.       Kila unapojiandaaa na jukumu kubwa ni muhimu kutanguliza maombi, Dr David Yong Cho wa kanisa la Full Gospel of Yoido kule Korea kusini huomba masaa matatu asubuhi kabla ya kuingia katika shughuli za kila siku, Martin Luther aliomba masaa matatu asubuhi kabla ya kuingia katika shughuli za kila siku Yesu mwana wa Mungu kwa maandalizi ya huduma yake alifunga na kuomba kwa siku 40 Luka 4:1-2, 14-15 “Na Yesu, hali amejaa Roho Mtakatifu, alirudi kutoka Yordani, akaongozwa na Roho muda wa siku arobaini nyikani, akijaribiwa na Ibilisi. Na siku hizo alikuwa hali kitu; hata zilipotimia, aliona njaa.” “Yesu akarudi kwa nguvu za Roho, akenda Galilaya; habari zake zikaenea katika nchi zote za kandokando. Naye alikuwa akifundisha katika masinagogi yao, akitukuzwa na watu wote.” 


4.       Ni muhimunpia kuwaamini wengine na kugawa majukumu si vema kila kitu ukakifanya wewe, kwa mamlaka uliyonayo unaweza kuwapa majukumu wengine na kuwaelekeza wakafanya kama ambavyo wewe ungefanya  Yesu aliwatuma wale 12 na wakafanya kazi nzuri wakamletea ripoti na akawaagiza wapumzike ona Marko 6:30-32 “Na mitume wakakusanyika mbele ya Yesu; wakampa habari za mambo yote waliyoyafanya, na mambo yote waliyoyafundisha. Akawaambia, Njoni ninyi peke yenu kwa faragha, mahali pasipokuwa na watu, mkapumzike kidogo. Kwa sababu walikuwako watu wengi, wakija, wakienda, hata haikuwapo nafasi ya kula.Wakaenda zao faragha mashuani, mahali pasipokuwa na watu.” Unaona Yesu alitambua kuwa watu wanaofanya hduma wabahitaji muda wa kuwa faragha na kupumzika 


5.       Kunapokuwa na mambo ya kuhuzunisha au habari ngumu pia huna budi kuhakikisha kuwa unajitenga na shughuli nyingi upate nguvu mpya Mathayo 14:1-13 “Wakati ule mfalme Herode alisikia habari za Yesu, akawaambia watumishi wake, Huyo ndiye Yohana Mbatizaji; amefufuka katika wafu; na kwa hiyo nguvu hizo zinatenda kazi ndani yake. Maana Herode alikuwa amemkamata Yohana, akamfunga, akamtia gerezani, kwa ajili ya Herodia, mke wa Filipo nduguye. Kwa sababu Yohana alimwambia, Si halali kwako kuwa naye. Naye alipotaka kumwua, aliwaogopa watu, maana walimwona Yohana kuwa nabii. Hata ilipofika sikukuu ya kuzaliwa kwake Herode, binti Herodia alicheza mbele ya watu, akampendeza Herode. Hata akaahidi kwa kiapo ya kwamba atampa lo lote atakaloliomba. Naye, huku akichochewa na mamaye, akasema, Nipe hapa katika kombe kichwa cha Yohana Mbatizaji. Naye mfalme akasikitika; lakini kwa ajili ya viapo vyake, na kwa ajili ya wale walioketi chakulani pamoja naye, akaamuru apewe; akatuma mtu, akamkata kichwa Yohana mle gerezani. Kichwa chake kikaletwa katika kombe, akapewa yule kijana; akakichukua kwa mamaye. Wanafunzi wake wakaenda, wakamchukua yule maiti, wakamzika; kisha wakaenda wakampasha Yesu habari. Naye Yesu aliposikia; hayo, aliondoka huko katika chombo, akaenda mahali pasipo watu, faraghani. Na makutano waliposikia, walimfuata kwa miguu kutoka mijini mwao.”


6.       Hatuwezi kufanya maamuzi muhimu huku tukiwa katika shughuli nyingi ni muhimu kukumbuka kuwa kila maamuzi muhimu yanahitaji maombi ili kwamba Mungu aweze kuingilia kati, viongozi nwengi sana wamefanya maamuzi mengi mabaya bila kufikiri wala kuwaza kwa sababu wako kwenye mtego wa shughuli nyingi kisha linawajia jambo linalohitaji maamuzi na wanaamua bila kuwa katika uwepo wa Mungu  Yesu alipotaka kuamua hata kuchagua viongozi aliomba usiku kucha Luka 6:12-13 “Ikawa siku zile aliondoka akaenda mlimani ili kuomba, akakesha usiku kucha katika kumwomba Mungu. Hata kulipokuwa mchana aliwaita wanafunzi wake; akachagua kumi na wawili miongoni mwao, ambao aliwaita Mitume;” 


7.       Tunapokuwa na Msongo wa mawazo inatupasa kuomba kwa masaa ya kutosha na hasa tunapotambua kuwa kuna mambio magumu mbeleni yanatukabili Luka 22:39-44 “Akatoka akaenda mpaka mlima wa Mizeituni kama ilivyokuwa desturi yake; wanafunzi wake nao wakafuatana naye. Alipofika mahali pale aliwaambia, Ombeni kwamba msiingie majaribuni. Mwenyewe akajitenga nao kama kiasi cha kutupa jiwe, akapiga magoti akaomba, akisema, Ee Baba, ikiwa ni mapenzi yako, uniondolee kikombe hiki; walakini si mapenzi yangu, bali yako yatendeke. Malaika kutoka mbinguni akamtokea akamtia nguvu. Naye kwa vile alivyokuwa katika dhiki, akazidi sana kuomba; hari yake ikawa kama matone ya damu yakidondoka nchini.]” 


8.       Kumbuka wakati wote Maombi ndiyo yanayotuweka karibu na Mungu, kusoma neno la ke na kulitafakari na kumtii yeye hutupa nguzu za rohoni kwa hiyo ni muhimu sana kwetu kuhakikisha kuwa tunaufurahia uwepo wa Mungu zaidi ya kukubali kuwa na shughuli nyingi Luka 5:16 “Lakini yeye alikuwa akijiepua, akaenda mahali pasipokuwa na watu, akaomba."  

         
Kama tutakuwa na shughuli nyingi na Mungu, Mungu ataweka wepesi katika yale tunayoyashughulikia kwa hiyo tusikubali kuingia katika mtego wa shughuli Nyingi

Mchungaji: Innocent Kamote
Mkuu wa wajenzi mwenye Hekima         

Hakuna maoni: