Jumatatu, 25 Novemba 2019

Kizazi kisichomjua Mungu!

Waamuzi 2:10 “Tena watu wote wa kizazi hicho nao walikusanywa waende kwa baba zao; kikainuka kizazi kingine nyuma yao, ambacho hakikumjua Bwana, wala hawakuijua hiyo kazi ambayo alikuwa ameitenda kwa ajili ya Israeli.” 

 
Wayahudi wa Madhehebu ya Orthodox huhakikisha kuwa watoto wao wanajua historia yao, dini yao mila zao na desturi zao, na kila mtoto huweza nkuelezea kuhusu familia yake hata vizazi kumi vilivyopita!

Utangulizi!


Katika moja ya tatizo kubwa ambalo jamii kubwa ya leo tumefeli duniani ni eneo la Malezi ya watoto, ni wazazi wachache sana ambao leo wamefanikiwa kuwaelekeza watoto wao na wakawa kama vile Mungu pamoja na wazazi walivyokusudia. Leo hii watu wengi sana wanalia na wameshindwa kuwadhibiti watoto, Namshukuru Mungu kuwa ameniita katika huduma ya kuwahudumia watoto, kwa miaka kadhaa sasa nimekuwa mkuu wa shule ya Sekondari Living Stone Boys’ Seminary, huku vilevile nikiwa Mchungaji wao, Najua na nimeona jinsi vijana wengi wanavyopoteza muelekeo hasa kwa sababu, ya kukosa malezi, wazazi wengi leo wako busy na utafutaji wa mali, wako busy na simu na ufuatiliaji wa Tamthilia na wameshindwa kujihusisha hata kidogo na maisha ya watoto, na wakati mwingine wamewasukumia shuleni, ili kwamba sisi walimu tuhangaike na watoto hawa ambao mimi huwaita kizazi cha ma-house girl Kizazi cha wadada wa kazi. Hili ni tatizo kubwa mno.


Tofauti ya kizazi wakati wa Joshua na kizazi wakati wa waamuzi.  


Kitabu cha waamuzi ni kitabu cha nyakati za mpito wa historia ya wana wa Israel baada ya uongozi wa Yoshua, tunakumbushwa katika maandiko na katika kitabu hiki kuwa watu walimtumikia Mungu wakati wote wa Yoshua, Na kuwa Mungu aliwabariki watu wake, 

Yoshua 24:31 “Nao Israeli wakamtumikia Bwana siku zote za Yoshua, na siku zote za hao wazee walioishi baada ya kufa kwake Yoshua, hao walioijua kazi yote ya Bwana, aliyowatendea Israeli.” 

Lakini kwenye kitabu hiki watu waliitumikia miungu na kuabudu sanamu, waliziacha kabisa njiia za Mungu na walisahahu kabisa matendo ya Mungu wala hawakujua matendo yake wala njia zake, Ndio maana biblia inasema kikainuka kizazi kingine kisichomjua Mungu! 

Waamuzi 2:10 “Tena watu wote wa kizazi hicho nao walikusanywa waende kwa baba zao; kikainuka kizazi kingine nyuma yao, ambacho hakikumjua Bwana, wala hawakuijua hiyo kazi ambayo alikuwa ameitenda kwa ajili ya Israeli.” 


Kwanini tunaona tofauti kati ya kizazi kile na kizazi hiki? Hawa wote walikuwa wana wa Israel, wote walilellewa na kukulia katika historia ya matendo ya Mungu, kuna tofauti kadhaa


1.       Kizazi kile kilichomtumikia Mungu walikuwa chini ya uongozi wa Yoshua ambaye alimtumikia Mungu kwa moyo wake wote na waliona matendo makuu ya Mungu

a.       Waliona Israel wakivuka mahali pakavu wakati mto wa Yordani ukiwa umefurika
b.       Waliona kuta za Yeriko zikianguka kwa uwezo mkubwa wa Mungu na melekezo yake
c.       Waliona Mungu akiwapigania dhidi ya wafalme watano wa waamori na Mungu akiwashushia matofali ya moto
d.       Waliona Mungu akiongeza Muda kwa Joshua na majeshi yake kwa kusimamisha jua
e.       Maadui walitiishwa dhidi yao, kilikuwa ni kizazi kilichojua na kuyaona matendo ya Mungu
f.        Walipitia magumu mengi na kujitoa sana, kilikuwa ni kizazi cha mashujaa waliojipatia ardhi ya mkanaani.

2.      Kizazi kilichofuata kilikuwa ni kizazi kingine ambachoi hawakumjua Mungu wala matendo yake

a.       Walisikia tu Historias ya matendo ya zamani, waliona tu nguzo za kumbukumbu za baba zao kuwa walipita pakavu Jordani
b.       Waliona tu Magofu ya mji wa Yeriko na walisikia tu kuwa ukuita ulianguka
c.       Walijishughulisha tu kuendeleza nchi ambayo Mungu aliwapa baba zao na wakasahu mambo ya Mungu mwenyewe
d.       Walikaa katika miji ambayo wala hawakuihangaikia, walikula matunda ya mizabibu ambayo hawakuilima
e.       Walikuwa wakifurahia tu utajiri na mafanikio ambayo baba zao waliyapata kutoka kwa maadui kama nyara walizoteka
f.        Hawakujua habari za Mungu kuigawa bahari ya shamu, hawakujua habari za Mungu Kushuka katika mlima wa Sinai na kuwapa amri kumi na sheria na taratibu nyingine


Sababu kuu ya kizazi hiki kutokumjua Mungu.


Ni muhimu kufahamu kuwa Mungu hapa sio tatizo, lakini kizazi kile kilichopita ndio kilikuwa tatizo, waoa hawakufanya yaliyo wajibu wao kwa Bwana, Mungu alikuwa amekusudia Israel wawafundishe watoto wao njia zake zote na kuwakumbusha matendo yake yote 


Kumbukumbu la Torati 6:1-14 “ Na hii ndiyo sheria, na amri, na hukumu, alizoziamuru Bwana, Mungu wenu, mfundishwe, mpate kuzitenda katika nchi ile mnayoivukia kuimiliki; upate kumcha Bwana, Mungu wako, kushika amri zake zote, na sheria zake, ninazokuamuru, wewe na mwanao, na mwana wa mwanao, siku zote za maisha yako; tena siku zako ziongezwe. Sikiza basi, Ee Israeli, ukaangalie kuzitenda; upate kufanikiwa, mpate kuongezeka sana, kama Bwana, Mungu wa baba zako, alivyokuahidi, katika nchi ijaayo maziwa na asali. Sikiza, Ee Israeli; Bwana, Mungu wetu, Bwana ndiye mmoja. Nawe mpende Bwana, Mungu wako, kwa moyo wako wote, na kwa roho yako yote, na kwa nguvu zako zote. Na maneno haya ninayokuamuru leo, yatakuwa katika moyo wako; nawe uwafundishe watoto wako kwa bidii, na kuyanena uketipo katika nyumba yako, na utembeapo njiani, na ulalapo, na uondokapo. Yafunge yawe dalili juu ya mkono wako, nayo yatakuwa kama utepe katikati ya macho yako. Tena yaandike juu ya miimo ya nyumba yako, na juu ya malango yako. Tena itakuwa atakapokwisha Bwana, Mungu wako, kukuleta katika nchi aliyowaapia babu zako, Ibrahimu na Isaka na Yakobo, ya kuwa atakupa; miji mikubwa mizuri usiyoijenga wewe,  na nyumba zimejaa vitu vyema vyote usizojaza wewe, na visima vimefukuliwa usivyofukua wewe, mashamba ya mizabibu na mizeituni usiyoipanda wewe, nawe utakula na kushiba; ndipo ujitunze, usije ukamsahau Bwana aliyekutoa nchi ya Misri, nyumba ya utumwa. Mche Bwana, Mungu wako; ndiye utakayemtumikia, na kuapa kwa jina lake. Msifuate miungu mingine katika miungu ya mataifa wawazungukao;”


Musa ni kama alikuwa ana wa zoom wana wa Israel aliwaonya mapema kwa neno la Mungu kuwa ni lazima wawaelimishe watoto wao na kuhakikisha kuwa wanampenda Mungu, ilikuwa ni kwa namna mbalimbali Mungu alitaka maswala haya ya msingi yakumbukwe, kizazi na kizazi walipaswa kufundishana kwa bidii matendo yote na maneno yote ya Mungu na kuwa kila kizazi wakumbuke, kile ambacho Mungu alikuwa amekikusudia wampende na kumtumikia. Mungu alirejea jambo kama hili kwa Yoshua kwa sababu Moyonimwake Mungu alikuwa anataka kizazi kipya kiyajue matendo yake ili wamuabudu


Yoshua 4:1-8 “Ikawa, hapo hilo taifa zima lilipokuwa limekwisha vuka Yordani, ndipo Bwana akanena na Yoshua, akamwambia, Haya, twaeni watu waume kumi na wawili katika hao watu, kila kabila mtu mmoja, kisha uwaamrishe, kusema, Twaeni mawe kumi na mawili, hapo katikati ya Yordani, mahali hapo miguu ya hao makuhani iliposimama imara, mwende nayo mawe hayo, mkayaweke nchi kambini, hapo mtakapolala usiku huu. Basi Yoshua akawaita hao watu kumi na wawili, aliokuwa amewaweka tayari tangu hapo, katika wana wa Israeli, kila kabila mtu mmoja; naye Yoshua akawaambia, Haya, piteni ninyi mtangulie mbele ya sanduku la Bwana, Mungu wenu, mwende pale katikati ya Yordani, mkatwae kila mtu wenu jiwe moja begani mwake, kwa kadiri ya hesabu ya kabila za wana wa Israeli; ili kwamba jambo hili liwe ishara kati yenu, hapo watoto wenu watakapowauliza ninyi katika siku zijazo, wakisema, Ni nini maana yake mawe haya? Ndipo mtakapowaambia, Ni kwa sababu maji ya Yordani yalitindika mbele ya sanduku la agano la Bwana; hapo lilipovuka Yordani, hayo maji ya Yordani yalitindika; na mawe haya yatakuwa ni ukumbusho kwa wana wa Israeli milele. Basi wana wa Israeli walifanya vile vile kama Yoshua alivyowaamuru, nao wakatwaa mawe kumi na mawili pale katikati ya Yordani, kama Bwana alivyomwambia Yoshua, sawasawa na hesabu ya kabila za wana wa Israeli; wakayachukua wakavuka nayo hata mahali pale walipolala, nao wakayaweka nchi kuko huko.” 


Unaweza kuona mkakati wa Mungu ni kuwa kila kizazi kiyajue matendo yake, watu wazima wawafundishe vija nana watoto kumjua Mungu, kuyajua matendo yake ili kwamba wampende Mungu na kumtumikia na kuacha kuabudu miungu, tatizo kubwa la kuibuka kwa kizazi kisichomjua Mungu ni kizazi kile kilichokuwa kikifurahia baraka za Mungu na kusahau kabisa wajibu wa kuwafunza watoto, leo hii dunia imejaa mafunzo ya ajabu mno, watu wanaohusika na ushoga wameandaa vijitabu vya kuwafundisha watoto ushoga mapema ili wauone kuwa ni kitu cha kawaida katika kizazi hiki, kanisa limepuuza maswala mazima ya kuwafundisha vijana na watoto, dini zimejikita katika maswala ya mafanikio utafutaji wa fedha na kutokushughulika na watoto ili kumtegenezea Yesu kanisa la baadaye matokeo kama haya na makosa kama haya ni sawa na yale waliyoyafanya wayahudi wakati wa waamuzi na matokeo yake wana wa Israel walijifunza tabia mbaya na kuabudu miungu na kumuacha Mungu aliye hai huku wakifanya maovu  angalia 

Waamuzi 2:11-13 “Wana wa Israeli walifanya yaliyokuwa ni maovu mbele za macho ya Bwana, nao wakawatumikia Mabaali. Wakamwacha Bwana, Mungu wa baba zao, aliyewaleta kutoka katika nchi ya Misri, wakafuata miungu mingine, baadhi ya miungu ya watu wale waliokaa karibu nao pande zote, wakajiinamisha mbele yao; wakamkasirisha Bwana, akaghadhibika. Wakamwacha Bwana, wakamtumikia Baali na Maashtorethi.” 


Leo hii kanisa linalia na manabii wa uongo, vuingozi wa kiroho wahuni, wasio na uadilifu, kuuzwa kwa mafuta, maji, sabuni, unga, chumvi, udongo na soda bangili za upako na kadhalika pamoja na kuweko kwa mafundisho ya ajabu ajabu tatizo kubwa sio wao tatizo kubwa ni kanisa lenyewe liliweka msingi gani katika kuwaandaa viongozi wa kiroho walio waadilifu? Unapolia na manabii wa uongo kumbuka kulina na walimju wa uongo waliowalea, kanisa lilikuwa wapi, wazazi walikuwa wapi jamii ilikuwa wapi wakati watoto wetu wanaharibika ? nani anawajibika? Ni sisi wenyewe Hatukujali mafundisho. Leo hii watu wametoa kipaumbele katika swala zima la kutafuta mafanikio ya kimwili na kusahau kujenga msingi wa kuifunza jamii juu ya swala zima la kumtafuta Mungu na kumpenda na kumpa kipaumbele na kumuabudu yeye na kuwa na hofu yake kamwe tusisahahu kuwa hukumu ya Mungu ipo  


2Petro 2:9-10 “basi, Bwana ajua kuwaokoa watauwa na majaribu, na kuwaweka wasio haki katika hali ya adhabu hata siku ya hukumu; na hasa wale waufuatao mwili katika tamaa ya mambo machafu. na kudharau mamlakaEndapo kanisa na wazazi hawatajali maswala mazima kuhusu ya kukilela kizazi kijacho katika njia za Mungu na uadilifu wake basi tujue kuwa hatutaweza kuiepuka hukumu ya Mungu, Zamani tulikuwa tunasema mauti imo sufuriani lakini sasa iko mdomoni ni lazima tuamke na kuwasaidia jamii yetu kujiandaa kumcha Mungu.

 
Jinsi ya kufanya ili kizazi kijacho kimjue Mungu


Wana wa Israel walikuwa na changamoto ambayo tunaweza kuigawa
·         Kizazi cha kwanza kioona matendo ya Mungu
·         Kizazi cha pili kilisikia matendo ya Mungu na
·         Kizazi chaa tatu hata kusikia hawakusikia 

1.       Tuwafundishe  kujenga na kuimarisha uhusiano na Mungu  Mungu alimchagua Ibrahimu kuwa rafiki yake kwa sababu alijua kuwa Ibrahimu atakuwa mwalimu mwema Mwanzo 18:17-19 “BWANA akanena, Je! Nimfiche Ibrahimu jambo nilifanyalo, akiwa Ibrahimu atakuwa taifa kuu, hodari, na katika yeye mataifa yote ya dunia watabarikiwa? Kwa maana nimemjua ya kwamba atawaamuru wanawe, na nyumba yake baada yake waishike njia ya BWANA, wafanye haki na hukumu, ili kwamba BWANA naye akamtimizie Ibrahimu ahadi zake.” 

    Kanisa, mzazi na walimu wanaotaka kuwa rafiki wa Mungu ni wale watakaokuwa wanajali kuwafundisha watoto na kizazi kijacho njia ya Mungu. Lazima kizazi kimoja kiwaeleze kizazi kijacho na kizazi kijacho kielezee wale wanaokuja  

      Yoel 1:2-3 “Sikieni haya, enyi wazee; Sikilizeni, enyi wenyeji wote wa nchi. Je! Mambo haya yamekuwako katika siku zenu, Au katika siku za baba zenu? Waarifuni watoto wenu habari yake, Watoto wenu wakawaambie watoto wao, Na watoto wao wakakiambie kizazi kingine.”


2.       Hakikisha kuwa unawaelimisha watoto kwa ghama yoyote Mithali 4:13 “Mkamate sana elimu, usimwache aende zake; Mshike, maana yeye ni uzima wako” kkatika kuhakikisha kuwa vijana wanapata Elimu na uadilifu ni lazima tukumbuke kuwa kuna walimu wakuu wanne, 1 Wazazi hawa ndio walimu wa kwanza, wao ndio msingi wa maisha ya kila kitu unapoona mwanao unajiona wewe waoni picha ya nyumbani kwao, 2. Shuleni, unampeleka katika shule ya aina gani, walimu wake wakoje ja wanamcha Mungu. Hakikisha kuwa watoto wanaosma kama huna ada fanya kazi na muombe Mungu aliyekupa hao watoto kwamba afungue mlango wa ada ili waende shule wasome, je ni nani anataka kuzaa house girl nani anataka kuzaa kuli, nani anataka kuza machinga, nani anataka kuzaa wazurulazi, wauza mayai tuwasomeshe tuwapatie elimu  3 Ibadani mwanao ataabudu wapi huyu ndio mwalimu wa ngazi ya juu kabisa hivyo lazima tuchague mahali sahihi kwa vija na wetu kujifunza mambo ya Mungu pia, 4 Shetani nimwalimu mbaya mno atawanyoosha wote ambao hawakuweka msingi unaoeleweka kwa vijana, kama kuna kitu tunapungukiwa Watanzania ni kutokuwaelimisha watoto wetu, Rafiki yangu mmoja alisema Japan ni inchi Tajiri na iliyoendelea sana kwa sababu waliwekeza katika elimu lakini hawana rasilimali nyingi kama tulionazo, na Tanzania ni inchi yenye rasilimali nyingi sana lakini tumepigwa na ukwasi kwa muda kwa sababu hatukuwa na maarifa ya kutosha, watoto wetu wanazaliwa na vipawa na karama na majaliwa makubwa sana lakini tunaweza kuyadidimiza kwa sababu tu tumeshindwa kuyachohcea kwa kutokuwapa maarifa yanayohitajika, tusiwapeleke watoto mbali na Mungu Yesu anawahitaji waje kwake Mathayo 19:14 “Lakini Yesu akasema, Waacheni watoto wadogo waje kwangu; wala msiwazuie; kwa maana walio mfano wa hao, ufalme wa mbinguni ni wao.”


3.       Usimnyime mtoto mapigo. 


Maandiko matakatifu yanataka kwanza tuutangulize upendo tuwapende vijana na watoto wetu kwa viwango ambavyo wataelewa kuwa tunawapenda, lakini tusiwadekeze, lazima watutii na watuheshimu, Biblia imesema lazima tufanye hayo, Padre mmoja aliyeitwa Don Bosco alisema atakwenda mtaani atakusanya vija na walioshindikana na atawakusanya na kuwapa elimu bila kuwachapa kiboko na watamtii, Padre huyu kutokana na mafanikio yake makubwa shule nyingi sana zimeanzishwa duniani na zinaitwa kwa jina lake Don Bosco kukumbuka uwezo wake mkubwa sana katika maswala ya nidhamu, lakini hata hivyo kama watoto hawasikii biblia imesema wapigwe viboko, sheria inayokataza watoto kuchapwa ni ya kishetani, kila dini inasema watoto waadhibiwe kuna sheikh hapa? Mtume Muhamad (SAW) alichapwa, alikuwa hajui kusoma na kuandika malaika jibril alipomtokea katika pango alimlazimisha asome na akariri kwa jila la mola wake “Iqraa bism rabik laz kalaaq” alilazimishwa mpaka aliugua aliumwa! Baada ya kulazimishwa kusoma, wewe lunasema viboko ni haramu? Mungu anasema  wacharazwe 

Mithali 13:24 “Yeye asiyetumia fimbo yake humchukia mwanawe; Bali yeye ampendaye humrudi mapema.”  Kila tabia mbaya tutakayoiona kwa watoto tuiondoe mapema kwa kuwacharaza, kuna matumaini kama tutawachapa kwa upendo bila kuzidi kiasi na kuwaumiza au tukiwa na hasira 

Mithali 19:18 “Mrudi mwanao, kwa maana liko tumaini; Wala usiikaze nafsi yako kwa kuangamia kwake.” Maandiko yanasema kuna matumaini tukiwadhibu kuna matumaini tukiwarudi, tena biblia inasema kwa kuwaadhibu tunaodoa ujinga ndani ya akili zao na mioyo yao na tunawaopa maarifa 

Mithali 22:15 “Ujinga umefungwa ndani ya moyo wa mtoto; Lakini fimbo ya adhabu itaufukuzia mbali.” Bilia inaonyesha kuwa fimbo itafukuzilia mbali ujinga kwa hiyo tusiwanyime adhabu tusiwanyime mapigo  

Mithali 23:13-14. “Usimnyime mtoto wako mapigo; Maana ukimpiga kwa fimbo hatakufa. Utampiga kwa fimbo, Na kumwokoa nafsi yake na Kuzimu.Biblia inasema hatakufa ukimchapa bali utaiokoa nafsi yake na kuzimu, ni fimbo ndio itaweka nidhamu, ni fimbo ndiyo itakayompa hekima na akili 

Mithali 29:15-17 “Fimbo na maonyo hutia hekima; Bali mwana aliyeachiliwa humwaibisha mamaye. Waovu wakiongezeka, maasi huongezeka; Bali wenye haki watayatazama maanguko yao. Mrudi mwanao naye atakustarehesha; Naam, atakufurahisha nafsi yako 

mtoto wako akiisha kujua nini mzazi anakitaka mapema sana atayashika mausia yako na utakuwa ni muongozo mkubwa utakaomsaidia kijana wako, atajua lipi jema na lipi baya, lazima tuwe na muda na watoto wetu na kuwaelekeza, na kuwafundisha utii, walekeze kuamkia watu wazima, walekeze kujilinda na maadui, waelekeze dalili za kujua mtu mwema na mtu mbaya, waelekeze kujisomea wewe mwenyewe ukiwa kielelezo cha hayo, mara nyingi watu hulaumu viongozi wa dini kuwa hawa jamaa wanahubiri tu lakini hawatendi sawa na kuhubiri kwao, haya yameanzia majumbani mzazi anamkataza mtoto wake kunywa pombe yeye mwenyewe anakunywa, unamkataza asivae mavazi ya kikahaba wewe mwenyewe unavaa, Lazima tujikite katika kuwalea waoto wetu kwa hali na mali, wasipotusikiliza baada ya hayo tutakuwa na uwezo wa kutoa Hesabu kwa Mungu, kuwa sisi tulijitahidi kufanya kila tuliloliweza kwaajili yao, lakini sehemu nyingine nilikuachia wewe Mungu na sitawajibika kama baba au mama aliyeshindwa kumpatia mtoto kile alichopaswa!


Na mkuu wa wajenzi mwenye Hekima
Rev. Innocent Kamote
0718990796

Jumapili, 24 Novemba 2019

Je mtu kama mimi Nikimbie?


Nehemiah 6:11Nami nikasema, Je! Mtu kama mimi nikimbie? Naye ni nani, akiwa kama nilivyo mimi, atakayeingia hekaluni ili kuponya maisha yake? Sitaingia.”



Utangulizi:

Nehemiah alikuwa moja ya viongozi  Muhimu sana aliyepewa Mzigo na Mungu wa kuujenga ukuta wa Yerusalem, Nehemia alikuwa ni kiongozi wa Pili aliyefanya kazi kubwa na ya muhimu ya kurejesha heshima ya mji wa Yerusalem, Mojawapo wa viongozi wakubwa waliotangulia alikuwa ni Zerubabel, Yeye alijenga Hekalu, na Ezra alikuja baadaye kwaajili ya kuwajenga watu kiroho, Lakini Nehemia alikuwa na kazi ya kuujenga ukuta wa Yerusalem kazi iliyokuwa muhimu kwaajili ya usalama wa watu wa Mungu na mji wa Mungu, Unaposoma kitabu hiki unaweza kudhani mwanzoni kuwa kazi hii ilikuwa Rahisi kwa sababu ilitoka kwa Mungu na Nehemiah alipewa kibali na Mungu


Nehemia 1:2-6 “Hanani, mmoja wa ndugu zangu, akanijia, yeye na watu wengine waliotoka Yuda; nami nikawauliza habari za Wayahudi waliopona, hao watu wa uhamisho waliosalia; na habari za Yerusalemu. Wakaniambia, Watu wa uhamisho, waliosalia huko katika wilaya ile, wamo katika hali ya dhiki nyingi na mashutumu; tena ukuta wa Yerusalemu umebomolewa, na malango yake yameteketezwa kwa moto. Hata ikawa niliposikia maneno hayo, nikaketi, nikalia, nikaomboleza siku kadha wa kadha; kisha nikafunga, nikaomba mbele za Mungu wa mbinguni; nikasema, Nakusihi, Ee Bwana, Mungu wa mbinguni, Mungu mkuu, mwenye kuogofya, mwenye kutimiza agano lake na rehema zake kwa hao wampendao na kuzishika amri zake; tega sikio lako, macho yako yakafumbuke, upate kuyasikiliza maombi ya mtumishi wako, ninayoomba mbele zako wakati huu, mchana na usiku, kwa ajili ya wana wa Israeli


Nehemia alikuwa ni mtu mwenye mzigo kwaajili ya Yerusalem, na alimuomba Mungu kwaajili ya Mzigo uliokuwa ndani yake na Mungu alimpa kibali, Biblia inaeleza kuwa mkono wa Mungu ulikuwa mwema juu yake Nehemia 2:18a “Nikawaeleza habari ya mkono wa Mungu wangu ulivyokuwa mwema juu yangu; yaani Mungu alikuwa amempa kibali kwaajili ya kazi ile na mfalme alimruhusu Nehemia na kumpatia kila kilichohitajika kwa ajili ya nyumba mji wa Yerusalem, hii ilikuwa ni kazi ngumu ni wito kwaajili yake


Hata hivyo kazi hii ilikuwa na vikwazo vingi na haikuwa rahisi, Shetani aliipinga kazi hii akitumia watu mbalimbali, kuitukana, kuidharau, kuinena vibaya na kuwatishia kina Nehemia ili yamkini aache kazi hii, wakatimwinguine walitaka kuwakatisha tamaa na kuwanenea maneno mabaya sana ya kudhoofisha pasipo sababu


Angalia


1.       Maadui walinena maneno ya kipuuzi mno kuhusu ujenzi wa ukuta ule Nehemia 4:1-3 “Lakini ikawa, Sanbalati aliposikia ya kwamba tulikuwa tukiujenga ukuta, akaghadhibika, akaingiwa na uchungu sana, akawadhihaki Wayahudi. Akanena mbele ya nduguze na mbele ya jeshi la Samaria, akisema, Wayahudi hawa wanyonge wanafanyaje? Je! Watajifanyizia boma? Watatoa dhabihu? Au watamaliza katika siku moja? Je! Watayafufua mawe katika chungu hizi za kifusi, nayo yameteketezwa kwa moto? Basi Tobia, Mwamoni, alikuwa karibu naye, akasema, Hata hiki wanachokijenga, angepanda mbweha, angeubomoa ukuta wao wa mawe.”


Nehemia alichokifanya wakati huu ilikuwa ni kuomba na kusonga mbele kwa kufanya kazi Nehemia 4:4-6 “Sikia, Ee Mungu wetu; maana tunadharauliwa; ukawarudishie mashutumu yao juu ya vichwa vyao, ukawatoe watekwe katika nchi ya uhamisho; wala usiusitiri uovu wao, wala isifutwe dhambi yao, mbele zako; kwa maana wamekukasirisha mbele ya hao wanaojenga. Basi tukaujenga ukuta; nao ukuta wote ukaungamanishwa kiasi cha nusu ya kimo chake; maana watu walikuwa na moyo wa kufanya kazi.”



2.       Maadui walipoona kuwa jamaa hawajakata tamaa bali waliendela na kazi wakashuriana kunazisha vita Nehemia 4:7-8 “Lakini ikawa, Sanbalati, na Tobia, na Waarabu, na Waamoni, na Waashdodi, waliposikia ya kuwa kazi ya kuzitengeneza kuta za Yerusalemu inaendelea, na ya kuwa mahali palipobomoka panaanza kuzibwa, basi wakaghadhibika mno; wakafanya shauri wote pamoja kuja kupigana na Yerusalemu, na kufanya machafuko humo.”



Nehemia alichokifanya sasa aliweka walinzi., na kazi iliendelea usiku na mchana walijenga huku kukiwa na walinzi kwaajili ya kuwapinga maadui Nehemia 4:9 “Bali sisi tulimwomba dua Mungu wetu, tena tukaweka walinzi, mchana na usiku, kwa sababu yao, ili kuwapinga.”



3.       Maadui walikusudia kuwashambulia wayahudi ili kuikomesha kazi ile kabisa Nehemia 4:10-12 Wakasema Yuda, Nguvu zao wachukuao mizigo zimedhoofika, na kifusi tele zipo; tusiweze kuujenga ukuta. Nao adui zetu wakasema, Hawatajua wala kuona, hata tutakapokuja kati yao, na kuwaua, na kuikomesha kazi hiyo. Kisha ikawa, Wayahudi walipokuja, wale waliokaa karibu nao, wakatuambia mara kumi, Kutoka kila mahali mtakaporejea watatushambulia.”



Nehemia hakukata tamaa yeye na watu wake waliendelea kujipanga waliweka ulinzi na kuhakikisha kuwa kazi inafanyika usiku na Mchana Nehemia 4:13-23.


4.       Baada ya Ibilisi kuona kuwa amewashindwa kwa namna hii alileta njaa, Familia za wayahudi wanawake na watoto walikopa fedha ili wapate chakula kwa sababu wanaume walikuwa na kazi ya kuujenga ukuta kule walikokopa walishikwa riba na hivyo umasikini mkubwa na njaa vikawapata Nehemia 5:1-6 “Ndipo kukatokea kilio kikuu cha watu, na wake zao, juu ya ndugu zao Wayahudi. Maana, walikuwako watu waliosema, Sisi, na wana wetu na binti zetu, tu wengi; na tupate ngano, tule, tukaishi. Tena walikuwako wengine waliosema, Tumeweka rehani mashamba yetu, na mizabibu yetu, na nyumba zetu; tupate ngano, kwa sababu ya njaa. Tena walikuwako wengine waliosema, Tumekopa fedha ili kulipa kodi ya mfalme kwa kuweka rehani mashamba yetu, na mizabibu yetu. Walakini miili yetu ni kama miili ya ndugu zetu, na watoto wetu kama watoto wao; kumbe! Mnawatia utumwani wana wetu na binti zetu kuwa watumishi, na baadhi ya binti zetu wamekwisha kutiwa utumwani; wala hatuwezi kujiepusha na hayo; maana watu wengine wana mashamba yetu na mizabibu yetu. Nami nilikasirika sana, niliposikia kilio chao, na maneno hayo.”


Nehemia hata hivyo tena aliwakemea viongozi kuwatoza riba wayahudi wenzao na kuamuru kuwarejeshea mashamba yao na kila kitu walichoweka Reheni Nehemia 5:7-19

5.       Mbinu ya mwisho kabisa shetani aliyoitumia ili sasa aweze kummaliza Nehemia ilikuwa ni kumtumia manabii wa uongo ili kwamba wamshawishi Nehemia avunje sheria za Kiyahudi na sheria za Kisrrikali wapate namna ya kumaliza, walituma watu nkumuita Nehemia mara kadhaa ili ikiwezekana akikubali kushuka waweze kumuua Nehemia 6:1-14, Hata hivyo Nehemia alikuwa na uwezo mkubwa mno wa kujijua mitego ya ibilisi na kuiepuka, Mungu alikuwa amempa Hekima ya kushinda vikwazo vyoye adui alikuwa amevikusudia, mwisho walipoona kuwa hawafanikiwi kumpata Nehemia wakamtumia Nabii wa uongo akamwambia kuna njama za wewe kutaka kuuuawa na Mungu anakutaka ukimbilie Hekaluni kujisalimisha  na walimshauri akimbilie Hekaluni akajifungie huko maana angauawa wakati wa usiku 

     Nehemia 6:8-12 “Ndipo mimi nikatuma kwake wajumbe, kusema, Hakukufanyika mambo kama hayo uyasemayo, lakini kwa moyo wako wewe mwenyewe umeyabuni. Kwani hao wote walitaka kutuogofisha, wakisema, Italegea mikono yao katika kazi, isifanyike. Lakini sasa nitaitia mikono yangu nguvu.  Nikaingia nyumbani kwa Shemaya, mwana wa Delaya, mwana wa Mehetabeli, aliyekuwa amefungwa; naye akasema, Tukutane nyumbani mwa Mungu, ndani ya hekalu, tukaifunge milango ya hekalu; kwa maana watakuja kukuua; naam, wakati wa usiku watakuja kukuua. Nami nikasema, Je! Mtu kama mimi nikimbie? Naye ni nani, akiwa kama nilivyo mimi, atakayeingia hekaluni ili kuponya maisha yake? Sitaingia. Nikatambua, na tazama, siye Mungu aliyemtuma; lakini amefanya unabii huu kinyume changu; nao Tobia na Sanbalati ndio waliomwajiri.”

      Nehemia alikuwa anajua sherai za Nchi na vilevile alikuwa anazijua sheria za Mungu Yeye alikuwa mtu wa kawaida tu na mtu wa kawaida kwa mujibu wa Torati hakupaswa kuingia Hekaluni na kujifungia kitendo hicho cha kuinhgia hekaluni na kujifungia katika chumba cha hekalu kilikuwa ni halali kwa Makuhani na ukoo wa kikuhani yaani walawi tu na mtu wa kawaida kama angeingia Hekaluni kwa mujibu wa Torati alitakiwa kuuawa Hesabu 18:7 “Nawe na wanao pamoja nawe mtautunza ukuhani wenu, kwa ajili ya kila kitu cha madhabahu, na kwa ajili ya vile vilivyomo ndani ya pazia, nanyi mtatumika. Nawapeni ukuhani kuwa utumishi wa kipawa; na mgeni akaribiaye atauawa.” 


Majaribu ya Nehemia yanatufundisha wazi kuwa shetani ataendela kutupinga kila wakati akitumia njia na mbinu na mashambulizi ya aina mbalimbali, ni lazima uelewe kuwa hata kama tuko katika mapenzi ya Mungu mambo hayawezi kuwa rahisi, kila wakati tuaona upinzani mkubwa adui atajaribu kutukatisha tamaa, atataka tushindwe atataka tuache kumuamini Mungu, ni muhimu kwetu kufahamu kuwa hatuna budi kusonga mbele, kuendela kuomba na kufanya kazi kwa bidii, na kumpuuzia ibilisi na kazi zake na wajumbe wake, Mungu anajua kile tunachokifanya kwamba twakifanya kwaajili ya utukufu nwake, hatutafuti sifa kwa wanadamu, Bali afadhali kupata sifa kwa Mungu, Mungu hataondoa upinzani kama ambavyo hakuondoa kwa Nehemia lakini wakati wote tukumbuke kuwa upinzani utatupeleka katika kiwango kingine, utatufanya tumtegemee Mungu zaidi kuliko akili zetu, tukikata tamaa tutakuwa tumeishia njiani, washndani wazuri ni wale wanaopambana mpaka dakika ya mwisho 

Tukifahamu kuwa shetani anatumia nini kutushambulia tutashinda kila aina ya kikwazo kinachokuja mbele yetu

Shetani atatumia 

1.       Hasira za wengine juu yako
2.       Dharau na kejeli
3.       Vitisho na mikwara
4.       Kukukatisha tamaa na kukuvunja moyo
5.       Kukuzungumzia kinyume
6.       Kukutisha
7.       Kuishiwa kiuchumi na kuwa na Madeni
8.       Kukutaka uvunje sheria  za nchi au shuleni
9.       Kukufanya ufanye dhambi


Hizi ndio mbinu alizozitumia kutaka kumkatisha tamaa Nehemia, lakini Nehemia alizijua zote alikaa katika maombi, alikaaa katika wito wake alioitiwa, Walijilinda na adui na walimtazama Mungu, Kama unamjua Yesu na unatimiza majukumu yako sawa na mapenzi yake ni lazima ujue kuwa utakutana na vikwazo,Kama umeitwa katika wito wowote au wewe ni kiongozi huna budi kufahamu kuwa kitakachokuokoa ni kuwa kama Nehemia kuomba, kuangalia kile ulichoitiwa, kujilinda na maadui na kumwangalia Mungu aliyekuita katika hilo uliloitiwa. Je mtu kama Mimi nikimbie? Naye ni nani atakayekuwa kama nilivyo atakayekimbia?


Nchi yetu hivi karibuni imeshuhudia upinzani wa kiuchumi hasa katika ameneo ya kuzuiwa kwa ndege zetu mara kwa mara na madui wa uchumi wa Taifa letu, jambo hili lisitukatishe tamaa, tuendelee kusonga mbele na kusimama na Mungu naye ataupigania. 

Na mkuu wa wajenzi mwenye Hekima
Rev. Innocent Kamote
0718990796

Alhamisi, 21 Novemba 2019

Ni zaidi ya Ukarimu!



Warumi 8:32Yeye asiyemwachilia Mwana wake mwenyewe, bali alimtoa kwa ajili yetu sisi sote, atakosaje kutukirimia na mambo yote pamoja naye?”


Utangulizi:

Moja ya sifa kubwa sana ya Mungu wetu ni pamoja na kuwa Mkarimu, Maandiko yanatufunza sisi nasi kuwa wakarimu,

Waebrania 13:2
Msisahau kuwafadhili wageni; maana kwa njia hii wengine wamewakaribisha malaika pasipo kujua.”  Lakini hata hivyo yanamfunua kuwa Mungu ni zaidi ya Ukarimu, hii inapimwa na andiko hili katika Warumi 8:32  Mstari huu unaakisi kinabii tendo lililofanywa na Abrahamu aliyekuwa na upendo mkubwa sana kwa Mungu kiasi cha kuwa tayari kumtoa Isaka.

Kimsingi na kinabii Ibrahimu alikuwa anamwakilisha Mungu na Isaka anamwakilisha Yesu, Tendo la Ibrahimu kuwa tayari kumtoa mwana wake wa pekee Isaka kwa Mungu, Hali kadhalika ni picha halisi ya namna na jinsi Mungu alivyokuwa mkarimu kiasi cha kuwa tayari kutoa  mwanaye wa pekee Yesu Kristo kwetu, na kwa ulimwengu mzima kwa ujumla  Yohana 3:16Kwa maana jinsi hii Mungu aliupenda ulimwengu, hata akamtoa Mwanawe pekee, ili kila mtu amwaminiye asipotee, bali awe na uzima wa milele.” Mungu yu aonyesha zaidi ya ukarimu kwa kumtoa mwanae wa Pekee Yesu Kristo kuja ulimwenguni kwa watu wasiofaa ili awaokoe huu ni zaidi ya ukarimu Yesu Kristo ni zawadi ya juu na kubwa mno ambayo tumepata kupewa kama wanadamu Isaya nabii anaielezea zawadi hii namna na jinsi Yesu alivyo zawadi kubwa mno na yenye thamani na nguvu ona!

Isaya 9:6-7 “Maana kwa ajili yetu mtoto amezaliwa, Tumepewa mtoto mwanamume; Na uweza wa kifalme utakuwa begani mwake; Naye ataitwa jina lake, Mshauri wa ajabu, Mungu mwenye nguvu, Baba wa milele, Mfalme wa amani. Maongeo ya enzi yake na amani Hayatakuwa na mwisho kamwe, Katika kiti cha enzi cha Daudi na ufalme wake; Kuuthibitisha na kuutegemeza Kwa hukumu na kwa haki, Tangu sasa na hata milele. Wivu wa Bwana wa majeshi ndio utakaotenda hayo.” 

    
Tumepewa Isaya anasema tumekarimiwa ni zawadi ya mtoto wa kipekee mwanamume, ni mfalme serekali iko mabegani mwake ni mshauri wa ajabu, ni Mungu mwenye nguvu na baba wa milele na mfalme wa amani, hana mwanzo wala mwisho ataketi katika kiti cha enzi cha Daudi, Huyu ni Yesu Kristo ni zawadi kubwa mno ni zawadi ya kipekee sana ni zawadi kubwa Mungu kutupa Yesu ameonyesha zaidi ya Ukarimu

Huu ni upendo mkubwa mno kwa kupewa Yesu Kristo kuwa zawadi kubwa kwetu:-
·         Hakuna wa kutushitaki
·         Hakuna wa kutuhukumu
·         Hakuna wa kututenga na upendo wa Mungu ulio katika Kristo Bwana wetu
Orodhesha chochote unachoweza kuorodhesha hakuna kinachoweza kulinganishwa na upendo wa Mungu kwetu na ukarimu wake wa kupita kawaida


Warumi 8:33-39 inasema “Ni nani atakayewashitaki wateule wa Mungu? Mungu ndiye mwenye kuwahesabia haki. Ni nani atakayewahukumia adhabu? Kristo Yesu ndiye aliyekufa; naam, na zaidi ya hayo, amefufuka katika wafu, naye yuko mkono wa kuume wa Mungu; tena ndiye anayetuombea.  Ni nani atakayetutenga na upendo wa Kristo? Je! Ni dhiki au shida, au adha, au njaa, au uchi, au hatari, au upanga? Kama ilivyoandikwa, ya kwamba, Kwa ajili yako tunauawa mchana kutwa, Tumehesabiwa kuwa kama kondoo wa kuchinjwa. Lakini katika mambo hayo yote tunashinda, na zaidi ya kushinda, kwa yeye aliyetupenda. Kwa maana nimekwisha kujua hakika ya kwamba, wala mauti, wala uzima, wala malaika, wala wenye mamlaka, wala yaliyopo, wala yatakayokuwapo, wala wenye uwezo, wala yaliyo juu, wala yaliyo chini, wala kiumbe kinginecho chote hakitaweza kututenga na upendo wa Mungu ulio katika Kristo Yesu Bwana wetu.”

Sasa basi ikiwa upendo wa Mungu kwetu ni mkubwa namna hii Paulo mtume anasema kwamba Kama Mungu alimuachilia mwana wake wa pekee kwaajili yetu atashindwaje kutukirimia na mambo mengine? Atatukarimia mambo yote pamoja naye, kama ametupa Yesu Kristo ni rahisi, kupewa  Mume, ni rahisi kupewa mtoto, ni rahisi kupewa ufaulu katika mitihani yako, ni rahisi kupewa gari, ni rahisi kupewa nyumba, ni rahisi kupewa Hekima


1Wafalme 3:5-13 “Na huko Gibeoni Bwana akamtokea Sulemani katika ndoto ya usiku; Mungu akamwambia, Omba utakalo nikupe. Sulemani akasema, Umemfanyia mtumwa wako Daudi baba yangu fadhili kuu, kadiri alivyoenenda mbele zako katika kweli, na katika haki, na katika unyofu wa moyo pamoja nawe; nawe umemwekea na fadhili hii kubwa, maana umempa mwana wa kuketi kitini pake kama ilivyo leo. Na sasa, Ee Bwana, Mungu wangu, umenitawaza niwe mfalme mimi mtumwa wako badala ya Daudi baba yangu; nami ni mtoto mdogo tu; sijui jinsi inipasavyo kutoka wala kuingia. Na mtumwa wako yu katikati ya watu wako uliowachagua, watu wengi wasioweza kuhesabiwa, wala kufahamiwa idadi yao, kwa kuwa ni wengi. Kwa hiyo nipe mimi mtumwa wako moyo wa adili niwahukumu watu wako, na kupambanua mema na mabaya; maana ni nani awezaye kuwahukumu hawa watu wako walio wengi? Neno hili likawa jema machoni pa Bwana, ya kuwa Sulemani ameomba neno hili. Mungu akamwambia, Kwa kuwa umeomba neno hili, wala hukujitakia maisha ya siku nyingi; wala hukutaka utajiri kwa nafsi yako; wala hukutaka roho za adui zako; bali umejitakia akili za kujua kuhukumu; basi, tazama, nimefanya kama ulivyosema. Tazama, nimekupa moyo wa hekima na wa akili; hata kabla yako hapakuwa na mtu kama wewe, wala baada yako hatainuka mtu kama wewe. Na mambo yale usiyoyaomba nimekupa, mali na fahari, hata hapatakuwa na mtu katika wafalme kama wewe, siku zako zote.”

Suleimani aliomba Hekima lakini Mungu alimuongezea Utajiri na heshima kubwa sana, Mungu alidhihirisha kuwa yeye ni zaidi ya ukarimu, yeye anaweza kutupa lolote tuliombalo na tulitakalo kwa kadiri ya wingi wa rehema zake na neema yake,  Yesu ni zaidi ya Hekima, Yesu ndio Hekima yenyewe kutoka Mbinguni unapokuwa naye unakuwa na kila kitu, Ukimtafuta yeye mambo mengine yote utazidishiwa, Yesu ndio zawadi ya juu kabisa ambayo Mungu amepata kuwapa wanadamu, nyingine ni ndogo Yesu ni zawadi kubwa mno sasa  Kama Mungu ametupa Yesu Kristo ni wazi kuwa ametupa kila kitu hatatuzuilia maswala mepesi tuyaombayo kwa kuwa amekwisha tenda jambo zito kuliko yote kutupa Yesu Kristo kama zawadi ya pekee ni kwaajili ya sababu hii nzito Paulo mtume anahoji kuwa kama Mungu hakumuachilia Yesu Kristo mwana wake wa pekee alimtoa kwaajili yetu, atakosaje atashindwaje atasitaje kutukirimia mambo yote pamoja naye kumbuka kuwa mambo yote pamoja naye yaani ukisha kuwa na Kristo ambaye ndiye mfalme wa Ufalme wa mbinguni hutakosa kamwe kupewa mengineyo huu ni zaidi ya ukarimu!


Warumi 8:32Yeye asiyemwachilia Mwana wake mwenyewe, bali alimtoa kwa ajili yetu sisi sote, atakosaje kutukirimia na mambo yote pamoja naye?”

Ni zaidi ya Ukarimu
Na Mkuu wa wajenzi mwenye hekima
Rev. Innocent Kamote
0718990796.