Jumatatu, 23 Novemba 2020

Mzeituni umeao katika nyumba ya Mungu!

Zaburi 52:8 “Bali mimi ni kama mzeituni Umeao katika nyumba ya Mungu. Nazitumainia fadhili za Mungu milele na milele.”



Utangulizi:

Ni muhimu kufahamu kuwa Mungu katika hekima yake alipouumba ulimwengu, aliiuumba ili uwe zawadi kubwa kwa wanadamu,  na aliweka miti na mimea kwaajili ya uhai na utatuzi wa matatizo ya kiafya kwa wanadamu, kwa msingi huo basi utaweza kuona kuwa, Miti ina uhusiano mkubwa wa uhai maisha na hata nafsi ya mwanadamu Lakini miti pia ina uhusiano wa kiroho na maisha ya mwanadamu. Mungu aliitoa miti na mimea kama zawadi kwa wanadamu kwaajili ya kunufaisha maisha yao ona Mwanzo 1:29 “Mungu akasema, Tazama, nimewapa kila mche utoao mbegu, ulio juu ya uso wa nchi yote pia, na kila mti, ambao matunda yake yana mbegu; vitakuwa ndivyo chakula chenu;

Katika miti au miche ambayo ilitolewa kama zawadi kwa wanadamu moja ya mti wa ajabu sana wenye nguvu za mwilini na rohoni ni mti wa Mzeituni, mti huu ni malimbuko ya amani ya dunia ni ni mti wa kwanza kutajwa mara baada ya gharika wakati wa nabii Nuhu, ukiacha mti wa mtini ambao ulitajwa mapema sana mara baada ya anguko la mwanadamu ona Mwanzo 8:6-12 “Ikawa baada ya siku arobaini, Nuhu akalifungua dirisha la safina, alilolifanya; akatoa kunguru, naye akatoka akaenda huko na huko, hata maji yakakauka juu ya nchi. Kisha akatoa njiwa, aone kwamba maji yamepunguka usoni pa nchi; bali yule njiwa hakuona mahali pa kutua kwa wayo wa mguu wake, akamrudia Nuhu safinani, maana maji yalikuwa juu ya uso wa nchi yote; naye akanyosha mkono, akamtwaa, akamwingiza mle safinani. Akangoja na siku saba tena; kisha akamtoa yule njiwa katika safina mara ya pili, njiwa akamjia jioni, na tazama, alikuwa na jani bichi la mzeituni kinywani mwake, ambalo amelitunda, basi Nuhu akajua ya kwamba maji yamepunguka juu ya nchi. Akangoja na siku saba tena, akamtoa yule njiwa; naye asimrudie tena kamwe.

Mungu aliweka uwezo wa ajabu katika mti huu, na miongoni mwa miti inayofanya kazi ya kuleta heshima kwa Mungu na wanadamu Mzeituni ni mojawapo ni mti  wa kwanza katika miti hiyo  maarufu ya kibiblia angalia Waamuzi 9:8-12 “Siku moja miti ilitoka ili kuutia mmoja mafuta uwe mfalme juu yao; ikauambia mti mzeituni, Tawala wewe juu yetu. Lakini huo mzeituni ukaiambia, Je! Niache mafuta yangu, ambayo kwangu mimi watu wamheshimu Mungu na wanadamu, ili niende nikayonge-yonge juu ya miti? Kisha miti ikauambia mtini, Njoo wewe, utawale juu yetu. Lakini huo mtini ukaiambia, Je! Niuache utamu wangu, na matunda yangu mazuri, niende nikayonge-yonge juu ya miti? Kisha miti ikauambia mzabibu, Njoo wewe, utawale juu yetu.

Sifa za mti wa Mzeituni!

Moja ya sifa ya mti wa Mzeituni ni kuwa ni mti wenye uwezo mkubwa sana wa kustahimili ukame, lakini ni mti usioweza kufa, ni mti wenye uwezo wa kufufuka, mizizi yake ina uwezo mkubwa sana wa kwenda chini na kujiunganisha na maji, kwa sababu hiyo sio rahisi kuuua mzeituni, ukitaka kuuua lazima uchomoe mizizi yake na kuitenganisha na maji huko ardhini, hapo ndipo utaweza kuua, unaweza kuifyekelea mbali lakini baada ya muda fulani unachipua tena!

Mti huu ulitumika nyakati za Agano la kale kusimika watu waliokusudiwa kuwa watumishi wa Mungu katika Nyanja mbalimbali, kama Wafalme, Makuhani na manabii, ili mtu aweze kumtumikia Mungu katika nafasi hizo alipakwa mafuta ya mzeituni kwa maelekezo ya Mungu na maisha ya mtu huyo yalibadilika sana, Makanisa makubwa ya zamani kama Anglican na Kanisa Katoliki huyatumia mafuta ya mzeituni katika ibada za kipaimara na wakati wa kusimika viongozi wa kanisa wakiwemo makuhani wa madhehebu hayo, hii ni kwa sababu wanakumbuka huduma za kikuhani za kupoaka mafuta zilizokuwa zikifanywa na makuhani au manabii nyakati za agano la kale mifano ifuatayo itakusaidia kuelewa uhusiano wa kiroho ulioko kati ya mwanadamu na upako wa mafuta ya mzeituni unaokaribisha nguvu za Mungu Roho Mtakatifu! Ona  

1Samuel 10:1-7 “Ndipo Samweli akatwaa kichupa cha mafuta, akayamimina kichwani pake, akambusu, akasema, Je! Bwana hakukutia mafuta [uwe mkuu juu ya watu wake Israeli? Nawe utamiliki watu wa Bwana, na kuwaokoa na mikono ya adui zao; kisha hii itakuwa ishara kwako ya kuwa Bwana amekutia mafuta] uwe mkuu juu ya urithi wake.Utakapoondoka kwangu leo, utakutana na wanaume wawili karibu na kaburi la Raheli, katika mpaka wa Benyamini huko Selsa; nao watakuambia, Punda hao uliokwenda kuwatafuta wameonekana; na tazama, baba yako ameacha kufikiri habari za punda, anafikiri habari zenu, akisema, Nifanye nini kwa ajili ya mwanangu? Kisha utakwenda mbele kutoka hapo, na kufika kwa mwaloni wa Tabori, na hapo watu watatu watakutana nawe, wanaokwea kumwendea Mungu huko Betheli, mmoja anachukua wana-mbuzi watatu, na mwingine anachukua mikate mitatu, na mwingine anachukua kiriba cha divai; nao watakusalimu na kukupa mikate miwili; nawe utaipokea mikononi mwao. Baada ya hayo utafika Gibea ya Mungu, hapo palipo na ngome ya Wafilisti; kisha itakuwa, utakapofika mjini, utakutana na kundi la manabii wakishuka kutoka mahali pa juu, wenye kinanda, na tari, na kinubi, na filimbi mbele yao, nao watakuwa wakitabiri; na roho ya Bwana itakujilia kwa nguvu, nawe utatabiri pamoja nao, nawe UTAGEUZWA KUWA MTU MWINGINE. Basi, hapo ishara hizi zitakapokutukia, fanya kama uonavyo vema; kwa kuwa Mungu yu pamoja nawe.

1Samuel 16:1-13Bwana akamwambia Samweli, Hata lini utamlilia Sauli, ikiwa mimi nimemkataa asiwamiliki Israeli? Ijaze pembe yako mafuta, uende, nami nitakupeleka kwa Yese, Mbethlehemi; maana nimejipatia mfalme katika wanawe. Samweli akasema, Nawezaje kwenda? Sauli akipata habari, ataniua. Basi Bwana akasema, Chukua ndama pamoja nawe, ukaseme, Nimekuja ili kumtolea Bwana dhabihu. Ukamwite Yese aje kwenye dhabihu, nami nitakuonyesha utakayotenda; nawe utamtia mafuta yule nitakayemtaja kwako. Samweli akafanya hayo aliyosema Bwana, akaenda Bethlehemu. Wakaja wazee wa mji kumlaki, wakitetemeka, nao wakasema, Je! Umekuja kwa amani? Naye akasema, Naam, kwa amani; nimekuja kumtolea Bwana dhabihu; jitakaseni; njoni pamoja nami kwenye dhabihu. Akawatakasa Yese na wanawe, akawaita kwenye dhabihu.  Ikawa walipokuja, alimtazama Eliabu, akasema, Yakini masihi wa BWANA yupo hapa mbele zake.Lakini Bwana akamwambia Samweli, Usimtazame uso wake, wala urefu wa kimo chake; kwa maana mimi nimemkataa. Bwana haangalii kama binadamu aangaliavyo; maana wanadamu huitazama sura ya nje, bali Bwana huutazama moyo. Ndipo Yese akamwita Abinadabu, akampitisha mbele ya Samweli. Naye akasema, Bwana hakumchagua huyu. Ndipo Yese akampitisha Shama. Naye akasema, wala Bwana hakumchagua huyu. Yese akawapitisha wanawe saba mbele ya Samweli. Samweli akamwambia Yese, Bwana hakuwachagua hawa. Kisha Samweli akamwambia Yese, Watoto wako wote wapo hapa? Naye akasema, Amesalia mdogo wao, na tazama, anawachunga kondoo. Basi Samweli akamwambia Yese, Tuma watu, wamlete; kwa sababu hatutaketi hata atakapokuja huku. Basi akatuma mtu, naye akamleta kwao. Naye alikuwa mwekundu, mwenye macho mazuri, na umbo lake lilikuwa la kupendeza. Bwana akasema, Ondoka, umtie mafuta; maana huyu ndiye. Ndipo Samweli akaitwaa pembe yenye mafuta, akamtia mafuta kati ya ndugu zake; na ROHO YA BWANA IKAMJILIA DAUDI KWA NGUVU tangu siku ile. Basi Samweli akaondoka, akaenda zake Rama.”           

Katika Agano jipya ishara ya kupakwa mafuta inaweza kuwa mafuta halisi ya mzeituni au kuwekewa mikono na mtumishi wa Mungu aliyepakwa mafuta aliyewekwa wakfu, sio lazima yawe mafuta kama yale yaliyokaa katika pembe lakini Mchungaji aliyepakwa mafuta anaweza kukuwekea mikono na kutamka kusudi la kukuwekea mikono na ikawa sawa kabisa na kupakwa mafuta, lakini hata akikupaka mafuta halisi ya zeituni, bado uweza utakuwa uleule wa kuwekea mikono au kupakwa mafuta, Ndio maana Yesu hakuwekewa mikono lakini alipakwa mafuta na Mungu mwenyewe mara baada ya kubatizwa na Yohana Mbatizaji, mtu anapowekwa wakfu kwa kupakwa mafuta anakuwa mtu mwenye uweza wa kiungu ndani yake na kumfanya kuwa mtu wa tofauti! Ona tangazao la Yesu la kuwa mpakwa mafuta;-

Luka 4:18-19 “Roho wa Bwana yu juu yangu, Kwa maana amenitia mafuta kuwahubiri maskini habari njema. Amenituma kuwatangazia wafungwa kufunguliwa kwao, Na vipofu kupata kuona tena, Kuwaacha huru waliosetwa, Na kutangaza mwaka wa Bwana uliokubaliwa.”

Mungu anaporuhusu katika kanuni zake uwekewe mikono au upakwe mafuta unakuwa na uweza wa kiwokovu ndani yako na mungu anakupoa neema inayokuwezesha kuwatetea wengina na kutimiza majukumu yako ambayo Mungu anakuwa ameyakusudia

Mzeituni umeao katika nyumba ya Mungu!

Zaburi 52:1-9

Kwa nini kujisifia uovu, Ewe jabari? Wema wa Mungu upo sikuzote.

Ulimi wako watunga madhara, Kama wembe mkali, Ewe mwenye hila

Umependa mabaya kuliko mema, Na uongo kuliko kusema kweli.

Umependa maneno yote ya kupoteza watu, Ewe ulimi wenye hila.  

Lakini Mungu atakuharibu hata milele; Atakuondolea mbali; Atakunyakua hemani mwako; Atakung'oa katika nchi ya walio hai.

Nao wenye haki wataona; Wataingiwa na hofu na kumcheka;

Kumbe! Huyu ndiye mtu yule, Asiyemfanya Mungu kuwa nguvu zake.

 Aliutumainia wingi wa mali zake, Na kujifanya hodari kwa madhara yake.

Bali mimi ni kama mzeituni Umeao katika nyumba ya Mungu.

Nazitumainia fadhili za Mungu milele na milele.

Nitakushukuru milele kwa maana umetenda; Nitalingojea jina lako kwa kuwa ni jema; Mbele ya wacha Mungu wako.

 

Katika msitari wetu wa Msingi Mwandishi anaonyesha ya kuwa yuko mtu wa hila, mtu mwenye kiburi mwenye uwezo wa kupoteza watu, muovu  inaonekana mtu huyu ana madhara ni hodari na mwenye nguvu, anawaandama wanadamu anapigana nao ana hila bila shaka ni wazi kabisa mtu huyu ni Ibilisi anasimama kushindana na makusudi ya Mungu ndani ya kila mmoja wetu anataka kutuahribia anataka kutuumiza anataka kuweka jeraha katika mioyo yetu, anataka tushindwe, anazuia mafanikio yetu, anapoingana na makusudi ya mungu ndani yetu na ndani ya mwandishi wa zaburi hii ambaye ni Daudi.  Mwandishi anamkumbusha  mtu huyo (Shetani) kuwa Yuko Mungu mwenye nguvu kushinda yeye, anauwezo wa Kumuharibu milele, anauwezo wa kumfutilia mbali, na ana uwezo wa kumng’oa na Daudi anatabiri kuwa wenye haki watamcheka!  Watashangaa kwanini mtu huyu wa kiburi hakumfanya Mungu kuwa nguvu yake? Kwa nini alitumainia mali zake na kujifanya hodari kumbe hana nguvu! Daudi anaeleza kuwa mtu anayemtegemea Mungu anayeutumainia  wema wa Mungu anayetambua kuwa Mungu ni mwema siku zote yaani hata wakati wa nyakati ngumu au ndani ya jambo gumu bado Mungu ni mwema tu! Hao ni sawa na Mzeituni uliopandwa katika nyumba ya Mungu,  yaani wale wanaomtegemea Mungu na kuzitumainia nguvu zake  watamea katika nyumba ya Mungu yaani katika uwepo wa Mungu watastawi watahuishwa, kwa sababu wanategemea fadhili za Mungu wanalitizamia jina lile jema yaani jina la Yesu, hawa hawatatikiswa wala hawataogopa, wakikatwa wanachipua tena! huwezi kuwazibia wameunganishwa mizizi yao na chemichemi ya uzima na chanzo cha uhai ambaye ni Mungu!,  watu walioungwa na chemichemu ya uzima wanautazamia wema wa Mungu siku zote Zaburi 52:1, hao hawawezi kutikiswa hawaogopi wana jina wanalolitumainia wanakaa katika uwepo wa Mungu wanazitumainia fadhili za Mungu milele na milele hawa ni watu wasiowezekana

Ndugu  tunalo tumaini lisiloweza kutikiswa sisi ni kama Mzeituni unaomea katika nyumba ya Mungu. Kila anayemtegemea Mungu na anayezitegemea fadhili zake hapaswi kuogopa, hatupaswi kufadhaika maana sisi kama ilivvyo kwa daudi ni mzeituni unaomea katika Nyumba ya Mungu, Mizeituni huwa haifi, mizeituni huwa inadumu milele, mizizi yake imeungwa na chemic hemi za chini sana za maji, ili tutoweke ni mpaka wachomoe mizizi inayotuunganisha na fadhili za Mungu, Usiogope!

 

Rev. Innocent Kamote

Mkuu wa Wajenzi mwenye Hekima

0718990796

Jumapili, 8 Novemba 2020

Hamjui yatakayokuwako kesho!

Mstari wa Msingi: Yakobo 4:13-15 “Haya basi, ninyi msemao, Leo au kesho tutaingia katika mji fulani na kukaa humo mwaka mzima, na kufanya biashara na kupata faida; walakini hamjui yatakayokuwako kesho. Uzima wenu ni nini? Maana ninyi ni mvuke uonekanao kwa kitambo, kisha hutoweka. Badala ya kusema, Bwana akipenda, tutakuwa hai na kufanya hivi au hivi.”


Utangulizi:

Mojawapo ya swali muhimu sana ambalo kila mwanadamu mwenye akili timamu huwa anajiuliza ni kuhusu kesho  “future”  kwamba itakuwaje kesho, nini kinafuata baada ya haya? Nini kinakuja, nini kitatokea wiki ijayo, mwezi ujao, mwaka ujao na wakati mwingine tunaona giza, na kujiuliza je tutakuwa na furaha au tutakuwa na dhuruba? Ni nani anaishikilia kesho yetu? Je napaswa kuwa na matumaini au kuogopa?


Itakuwaje mtihani unaokuja mbele yetu? Tutapata habari gani, itakuwaje matokeo ya uchaguzi wa, nani atashinda na itakuwaje akishinda fulani? Itakuwaje kazini, itakuwaje ndoa yangu, itakuwaje marafiki zangu, itakuwaje familia yangu? Itakuwaje afya yangu? Itakuwaje nikistaafu? Itakuwaje nikiachwa?


Watu wengi sana wanaogopa sana kuhusu maisha yajayo na kwa sababu hii ingawa wanajua umuhimu wa maswali hayo lakini kutokana na hofu au woga kisaikolojia watu wengi huwa wanapotezea swali hili Muhimu ili kupata unafuu na kutuliza maumivu yake, Mungu anajua kwamba swala kuhusu kesho ni swali tata sana kwa wanadamu na hataki tuogope wala kujisumbua hususani tunapokuwa na uhusiano mwema na yeye  Yesu Kristo anawatoa hofu kabisa waaumini wake akitaka jambo hili lisiwasumbue ona


Mathayo 6:31-34 “Msisumbuke, basi, mkisema, Tule nini? Au Tunywe nini? Au Tuvae nini? Kwa maana hayo yote Mataifa huyatafuta; kwa sababu Baba yenu wa mbinguni anajua ya kuwa mnahitaji hayo yote. Bali utafuteni kwanza ufalme wake, na haki yake; na hayo yote mtazidishiwa. Basi msisumbukie ya kesho; kwa kuwa kesho itajisumbukia yenyewe. Yatosha kwa siku maovu yake.”


Kwa kuwa Mungu anajua kuwa swala la kesho itakuwaje ni swala zito kwa wanadamu Maandiko yanawafundisha watu wa Mungu namna inavyowapasa kuenenda, watu wenye kiburi na watu wasiomjua Mungu huwa wana uhakika sana na maisha ya kesho kunakosababishwa na majivuno na kiburi.


Neno la Mungu linaonya kujisifu kuhusu kesho!


Watu wasiomjua Mungu huwa na tabia ya kujisifu na kujivuna kuhusu Kesho! Jambo ambalo neno la Mungu limeonya sana kwa njia nyingi na kwa mifano mingi wako watu ambao hujivunia kesho kana kwamba wanajua yatakayotukia kesho Biblia inaonya vikali sana kuhusu maisha yajayo au kuhusu kesho ona Mithali 27:1 “Usijisifu kwa ajili ya kesho; Kwa maana hujui yatakayozaliwa na siku moja.Wako watu hujivunia kuhusu kesho kana kwamba wana uhakika nayo na wanamuweka pembeni Mungu katika mipango yao na makusudi yake, Neema yake na wema wake  wako watu ambao walisahau kuwa kila kitu na kila jambo liko kwenye mikono ya Mungu, Mungu ana namna yake ya kuwanyoosha watu wenye kiburi


Ø Daniel 4:28-33 “Hayo yote yakampata mfalme Nebukadreza. Baada ya miezi kumi na miwili, alikuwa akitembea ndani ya jumba la kifalme katika Babeli. Mfalme akanena, akasema, Mji huu sio Babeli mkubwa nilioujenga mimi, uwe kao langu la kifalme, kwa uwezo wa nguvu zangu, ili uwe utukufu wa enzi yangu? Hata neno lile lilipokuwa katika kinywa cha mfalme, sauti ilikuja kutoka mbinguni, ikisema, Ee mfalme Nebukadreza, maneno haya unaambiwa wewe; Ufalme huu umeondoka kwako.Nawe utafukuzwa mbali na wanadamu, na makao yako yatakuwa pamoja na wanyama wa kondeni; utalishwa majani kama ng'ombe, na nyakati saba zitapita juu yako, hata utakapojua ya kuwa Aliye juu ndiye anayemiliki katika ufalme wa wanadamu, naye humpa amtakaye, awaye yote. Saa iyo hiyo jambo hilo likatimizwa, likampata Nebukadreza; alifukuzwa mbali na wanadamu, akala majani kama ng'ombe, na mwili wake ulilowa maji kwa umande wa mbinguni, hata nywele zake zikakua, zikawa kama manyoya ya tai, na kucha zake kama kucha za ndege.“

 

Ø Matendo 12:20-23 “Naye Herode alikuwa amewakasirikia sana watu wa Tiro na Sidoni; wakamwendea kwa nia moja, na wakiisha kufanya urafiki na Blasto, mwenye kukitunza chumba cha mfalme cha kulalia, wakataka amani; kwa maana nchi yao ilipata riziki kwa nchi ya mfalme. Basi siku moja iliyoazimiwa, Herode akajivika mavazi ya kifalme, akaketi katika kiti cha enzi, akatoa hotuba mbele yao. Watu wakapiga kelele, wakisema, Ni sauti ya Mungu, si sauti ya mwanadamu. Mara malaika wa Bwana akampiga, kwa sababu hakumpa Mungu utukufu; akaliwa na chango, akatokwa na roho.


Ø Luka 12: 15-21 “Akawaambia, Angalieni, jilindeni na choyo, maana uzima wa mtu haumo katika wingi wa vitu vyake alivyo navyo. Akawaambia mithali, akisema, Shamba la mtu mmoja tajiri lilikuwa limezaa sana; akaanza kuwaza moyoni mwake, akisema, Nifanyeje? Maana sina pa kuyaweka akiba mavuno yangu. Akasema, Nitafanya hivi; nitazivunja ghala zangu, nijenge nyingine kubwa zaidi, na humo nitaweka nafaka yangu yote na vitu vyangu. Kisha, nitajiambia, Ee nafsi yangu, una vitu vyema vingi ulivyojiwekea akiba kwa miaka mingi; pumzika basi, ule, unywe, ufurahi. Lakini Mungu akamwambia, Mpumbavu wewe, usiku huu wa leo wanataka roho yako! Na vitu ulivyojiwekea tayari vitakuwa vya nani?Ndivyo alivyo mtu ajiwekeaye nafsi yake akiba, asijitajirishe kwa Mungu.”  

 

Ø Mjezi wa Meli ya TITANIC  ambayo ilikuwa meli ya kifahari sana iliyokuwa na viwanja vya mpira, kumbi za starehe na mabwawa ya kuogelea alipoulizwa kuhusu uimara wa meli hiyo alijigamba na kusema hata Mungu hawezi kuizamisha, meli hii ilizama siku ya nne tu tangu ilipoanza safari kutoka Uingereza baada ya kugonga mwamba wa barafu katika bahari ta Atlantic  mnamo asubuhi ya tarehe 15/04.1912, Meli hii ilikuwa na abiria wapatao 2240 na kati yao zaidi ya 1500 walipoteza maisha, hatujui kesho yetu, kila aina ya kile tunachokifikia duniani hatuna budi kukumbuka kuwa ni kwa neema ya Mungu tu!


Mifano hii yote katika Biblia imeandikwa ili kutuonya sisi wanadamu ya kwamba hatuna kesho, kujilimbikizia mali na kuwa na choyo hakuongezei uzima wetu duniani, kila aina ya mafanikio tuliyionayo hayatokani na uwezo wetu ni neema ya Mungu  na wema wake ona Paulo mtume ndiye mtume aliyefanya kazi kubwa kuliko mitume wote lakini wakati wote alikumbuka kuwa alifanya chini ya neema ya Mungu na sio uwezo wake ona  1Wakoritho 15:10 “Lakini kwa neema ya Mungu nimekuwa hivi nilivyo; na neema yake iliyo kwangu ilikuwa si bure, bali nalizidi sana kufanya kazi kupita wao wote; wala si mimi, bali ni neema ya Mungu pamoja nami.Tunapaswa kuhakikisha kuwa tunaitegemea neema ya Mungu na kumtukuza yeye katika kila jambo na kumtanguliza yeye, kila mmoja anapaswa kuhakikisha anajilinda na kiburi kwa vile maisha hayako katika mikono yetu! Na Hatujui yatakayokuwako Kesho!


Hamjui yatakayokuwako kesho! 


Hakuna ajuaye kesho, Kesho iko katika mikono ya Mungu, Mungu anajua yote kuhusu kesho, Mungu anajua kila kitakachotokea anajua kitakachotokea kesho, wiki ijayo, mwezi ujao na miaka ijayo kwa hiyo kesho iko katika mikono ya Mungu Isaya 46:9-10 “kumbukeni mambo ya zamani za kale; maana mimi ni Mungu, wala hapana mwingine; mimi ni Mungu, wala hapana aliye kama mimi; nitangazaye mwisho tangu mwanzo, na tangu zamani za kale mambo yasiyotendeka bado; nikisema, Shauri langu litasimama, nami nitatenda mapenzi yangu yote.” Mungu anautangaza mwisho tangu mwanzo, Mungu anakujua na wewe nawe anajua unayoyahitaji anajua utakuwa nani anajua atakayeolewa na wewe anajua utakayemuoa anajua utakuwa na watoto wangapi anajua mwanzo na hata mwisho wa maisha yetu, alitambua mwisho wa Yusufu na kuutangaza kwa njozi kabla,  Mungu alikuwa anajua kuwa mavazi ya Yesu yatapigiwa kura miaka 1000 kabla ya Yesu Daudi alitabiri kitakachompata Yesu ona Zaburi 22:18 “Wanagawanya nguo zangu, Na vazi langu wanalipigia kura.” na Mathayo 27:35 “Walipokwisha kumsulibisha, waligawa mavazi yake, wakipiga kura; [ili litimie neno lililonenwa na nabii, Waligawa nguo zangu kati yao, na juu ya vazi langu walipiga kura.]”  Mungu anaweza kutuambia hata leo akitaka kuhusu kesho yetu na hivyo kama tunamtegemea na kumuamini tunapaswa kuwa na unyenyekevu na kumtegemea yeye na kumtanguliza yeye na kumuomba yeye, Kesho yetu iko mikononi mwa Mungu hatupaswi kusahau hilo yeye amakuwepo tangu mwanzo na yuko hata milele, Yesu ni yeye yule jana leo na milele anajua kila kitu kitakachotokea  na anampango mwema kwa aajili ya kila mmoja anayemtanguliza na kumtegemea yeye Warumi 8:28-30 “Nasi twajua ya kuwa katika mambo yote Mungu hufanya kazi pamoja na wale wampendao katika kuwapatia mema, yaani, wale walioitwa kwa kusudi lake. Maana wale aliowajua tangu asili, aliwachagua tangu asili wafananishwe na mfano wa Mwana wake, ili yeye awe mzaliwa wa kwanza miongoni mwa ndugu wengi. Na wale aliowachagua tangu asili, hao akawaita; na wale aliowaita, hao akawahesabia haki; na wale aliowahesabia haki, hao akawatukuza.” 


Mkumbuke Mungu katika mipango yako yote. 


Ni muhimu kufahamu kuwa maandiko yanatufundisha kwamba tunapaswa kumtanguliza Mungu mbele katika kila jambo, katiia mipango yetu maono yetu ndote zetu na kazi zetu tunapaswa kumuomba Mungu na kumtanguliza yeye na hatupaswi kuzitegemea na kujivunia akili zetu wenyewe, Watu wenye kiburi hawa na choyo wadhalimu hujisifia tama zao na hawataki kumkumbuka wala kumtanguliza Mungu kwa namna yoyote ile Zaburi 10:2-3 “Kwa kiburi chake asiye haki mnyonge anafuatiwa kwa ukali; Na wanaswe kwa hila zizo hizo walizoziwaza. Maana mdhalimu hujisifia tamaa ya nafsi yake, Na mwenye choyo humkana Bwana na kumdharau.” 


Na. Rev. Innocent Kamote

Mkuu wa wajenzi mwenye Hekima !

0718990796