Jumatatu, 27 Februari 2023

Kunyamaza mbele ya wakata Manyoya!


Isaya 53:7-11 “Alionewa, lakini alinyenyekea, Wala hakufunua kinywa chake; Kama mwana-kondoo apelekwaye machinjoni, Na kama vile kondoo anyamazavyo Mbele yao wakatao manyoya yake; Naam, hakufunua kinywa chake.  Kwa kuonewa na kuhukumiwa aliondolewa; Na maisha yake ni nani atakayeisimulia? Maana amekatiliwa mbali na nchi ya walio hai; Alipigwa kwa sababu ya makosa ya watu wangu.  Wakamfanyia kaburi pamoja na wabaya; Na pamoja na matajiri katika kufa kwake; Ingawa hakutenda jeuri, Wala hapakuwa na hila kinywani mwake. Lakini Bwana aliridhika kumchubua; Amemhuzunisha; Utakapofanya nafsi yake kuwa dhabihu kwa dhambi, Ataona uzao wake, ataishi siku nyingi, Na mapenzi ya Bwana yatafanikiwa mkononi mwake; Ataona mazao ya taabu ya nafsi yake, na kuridhika. Kwa maarifa yake mtumishi wangu mwenye haki Atawafanya wengi kuwa wenye haki; Naye atayachukua maovu yao. Kwa hiyo nitamgawia sehemu pamoja na wakuu, Naye atagawanya nyara pamoja nao walio hodari; Kwa sababu alimwaga nafsi yake hata kufa, Akahesabiwa pamoja na hao wakosao. Walakini alichukua dhambi za watu wengi, Na kuwaombea wakosaji.”



Utangulizi;

Leo nataka kuzungumzia moja ya siri kubwa sana ya mafanikio yetu katika maisha ya kila siku na katika maisha yetu ya utumishi, katika uzoefu wangu wa maisha tangu utoto na nadhani hata kwa watoto wengine na mpaka tunakuwa huwa tumejengwa katika dhana ya kujifunza kujitetea  na kutokukubali kukaa kimya au kuonewa na mara nyingi sana watu huwa wanaweza kukuchochea usikubali kukaa kimya hasa unapoonewa na jamii inaweza kukuona wewe ni mjinga sana kama ulikuwa na uwezo wa kujitetea lakini wewe ukaamua kukaa kimya au kupoteza haki zako ni kama unaonekana wewe ni dhaifu, kwa hiyo mara kwa mara tunajifunza kujenga hioja za kujitetea lakini maandiko yanatufunza kanuni nyingine ya kipekee sana yenye nguvu mno katika maisha yetu na kanuni hii ni kutulia na kukaa kimya, hii ndio Kanuni iliyotumiwa na Mtu mkubwa zaidi aliyepata kuishi Yesu Kristo Mwana wa Mungu kama anavyoeleza Isaya wakati akiwa anaonewa yeye alitulia kama kondoo anavyoweza kutulia kwa wakatao manyoya ona

Isaya 53:7 “Alionewa, lakini alinyenyekea, Wala hakufunua kinywa chake; Kama mwana-kondoo apelekwaye machinjoni, Na kama vile kondoo anyamazavyo Mbele yao wakatao manyoya yake; Naam, hakufunua kinywa chake.“

Ufahamu kuhusu tendo la kukata manyoya

Kwa bahati mbaya sana Hapa kwetu Tanzania, hatuna jamii ya kondoo wa kukatwa manyoya, lakini katika nchi nyingi jamii ya kondoo wenye manyoa mengi wamekuwepo tangia miaka mingi sana ikiwemo katika Israel, na ndio maana Isaya aliyeishi miaka 700 kabla ya Kristo anaeleza jambo hili.

Kwa kawaida Kondoo wenye manyoya walikuwepo tangu zamani na miaka ya zamani sana swala la kukata manyoya lilikuwa ni swala la asili tu kondoo wenyewe wangeweza kujikwaruza kwenye miti na kuondoa uchafu na kujipunguza manyoya, lakini Manyoya ya kondoo yalipoanza kutumika kama bidhaa ya kutengeneza nguo, na shughuli nyingine wanadamu waliona wapandikize jamii ya kondoo watakaozalisha manyioya kwa wingi ili kupata faida na ndio kukawepo kondoo wenye manyoa maengi zaidi, kwa msingi huo manyoya haya yana faida kubwa sana kwa kondoo mwenyewe wakati wa baridi kuweza kukabiliana na hali joto la nchi manyoya huwasaidia kuwa salama wakati wa baridi na mara msimu wa baridi unapoisha, na kuanza msimu wa joto wakulima huwa na sherehe za kuwakata kndoo manyoya na kuvuna pamba nyingi inayotokana na kondoo, mwenye kondoo hupata faida lakini vilevile kondoo wanafaidika kuwa na afya nzuri na kujilinda na wadudu wanaoweza kusababisha magonjwa wakati wa joto, na hivyo kondoo hunyolewa kila mwaka mara moja angalau kwaajili ya haya , wakulima hufanya sherehe kubwa kama vile wamevuna mazao

1Samuel 25: 2-8 “Na huko Maoni kulikuwa na mtu mmoja, ambaye alikuwa na mali yake katika Karmeli; naye yule mtu alikuwa mkuu sana, mwenye kondoo elfu tatu na mbuzi elfu; naye alikuwa akiwakata manyoya kondoo zake huko Karmeli. Na jina la mtu huyo aliitwa Nabali; na jina la mkewe aliitwa Abigaili, na huyo mwanamke alikuwa mwenye akili njema, mzuri wa uso; bali yule mwanamume alikuwa hana adabu, tena mwovu katika matendo yake; naye alikuwa wa mbari ya Kalebu. Basi Daudi akasikia huko nyikani ya kuwa Nabali alikuwa katika kuwakata manyoya kondoo zake. Daudi akatuma vijana kumi, Daudi naye akawaambia hao vijana, Kweeni mwende Karmeli, na kumwendea huyu Nabali ili mnisalimie; na hivi ndivyo mtakavyomwambia huyu aishiye salama, Amani na iwe kwako, na amani nyumbani mwako, na amani kwao wote ulio nao. Nami sasa nimesikia ya kuwa una watu wanaokata manyoya kondoo zako; haya! Wachungaji wako wamekuwa pamoja nasi, wala hatukuwadhuru, wala hawakukosa kitu wakati wote walipokuwako huko Karmeli. Waulize vijana wako, nao watakuambia; basi na wakubaliwe vijana hawa machoni pako; maana tumekujia katika siku ya heri; uwape, nakusihi, cho chote kitakachokujia mkononi, uwape watumwa wako na mwanao Daudi.”

Unaona ? kwa msingi huo ukataji kondoo manyoya lilikuwa ni tukio lililoeleweka vema sana katika jamii ya waisrael kuliko kwetu Afrika ya mashariki na  maeneo mengine duniani, na kwa bahati njema kwa vile kondoo walizoea zoezi hili na kama wanyama wenyewe walivyo wapole walikubali na kuonyesha ushirikiano wakati wa kunyolewa na hivyo hakukuwa na kamata kamata na mikiki mikiki wakati wa kunyolewa na kondoo walitulia na kunyamaza mbele ya wakata manyoya! 

Ni katika mazingira kama haya Nabii Isaya anatabiri na kuonyesha ushujaa na utulivu mkubwa sana aliokuwa nao Yesu wakati wa mateso yake yeye alionewa na aliwekewa hata na mashahidi wa uongo na waliyoyazungumza hayakuwa na ukweli lakini Kristo alinyamaza kimya ona

 

Mathayo 27:11-14 “Naye Yesu akasimama mbele ya liwali; liwali akamwuliza, akasema, Wewe ndiwe mfalme wa Wayahudi? Yesu akamwambia, Wewe wasema. Lakini aliposhitakiwa na wakuu wa makuhani na wazee, hakujibu hata neno. Ndipo Pilato akamwambia, Husikii ni mambo mangapi wanayokushuhudia? Asimjibu hata neno moja, hata liwali akastaajabu sana.         

Kuna kitu kikubwa cha kujifunza kutoka kwa Yesu, wakati wa mateso yake na wakati wa kuhukumiwa kwake watu walipeleka mashitaka ya uongo na kumsingizia mambo mengi lakini yeye hakujibu neno, pamoja na kushutumiwa kwa mambo mengio namna hiyo mpaka Hakimu alishangaa ni mshitakiwa gani huyu asiyejitetea alikaa kimya sawa na alivyotabiri isaya kuwa Yesu alikuwa kama kondoo kayika mikono ya wakata manyoya

Kunyamaza ni Nidhamu

Kwa asili hakuna mwanadamu anaweza kukubaliana na kuchafuliwa jina lake na wakati mwingine unaweza kulazimika kumlipa mtu fedha nyingi kama akikufungulia kesi za madai na kudai fidia ya kuchafuliwa jina, kila mtu anapenda jina zuri, kila mwanadamu anapenda heshima na hakuna mtu anayefurahia kudhalilishwa  au kuchafuliwa jina lake na heshima yake

Mithali 22:1 “Heri kuchagua jina jema kuliko mali nyingi; Na neema kuliko fedha na dhahabu.” Unana kimsingi mtu anapochafuliwa jina kuna vitu vinawaka sana moyoni na unaweza kujikuta unataka kujibu na kujitetea  lakini uwezo wa kunyamaza na kutulia huonyesha uwezo mkubwa sana wa kinidhamu ulionao,  watu wakati mwingine wanaweza kukuharibia jina, wanaweza kukusema vibaya wanaweza kuzungumza maneno ya uongo na uzushi mkubwa sana, wanaweza kutengeneza skendo, wanaweza kueleza matetesi, kukusengenya, kukuchafua kukusema vibaya , kueleza maswala mabaya ambayo wakati mwingine ni kama ynaweza kufanana na ukweli kabisa, watu wanaweza kujenga dhana mbaya sana kukuhusu, Katika maisha yangu nimefanya kazi mbalimbali za injili nimefundisha vyuo vya biblia kwa miaka karibu 12, nimekuwa mchungaji kiongozi kwa maiaka zaidi ya 22 nimekuwa mkuu wa shule na kuwasaidia wanafunzi kiroho na kitaaluma wakati mwingine nimewahi kusikia habari zangu zikizungumzwa sio za kazi ya injili niliyoifanya bali ya mambo mabaya yanayosaikiwa kuwa nimeyafanya,  watu wanazungumza mabaya kunihusu, sio jambo jepesi kukaa kimya, inahitaji nidhamu, nampenda sana Muhubiri Mtume Mwamposa moja ya vitu ninavyopenda kuhusu yeye sina cha kusema kuhusu huduma zake, kuhusu maji au mafuta lakini Muhubiri huyu huwa hajibu kitu chochote wala neno lolote la mtu yeyote anayemshutumu kwa jambo lolote  hii ni nidhamu ya hali ya juu je HUSIKII NI MAMBO MANGAPI WANAYOKUSHUHUDIA?  Aliuliza Liwali kwa Yesu lakini Bwana Yesu alikaa kimya kuna kanuni gani muhimu katika kukaa kimya nini tunaweza kujifunza kutoka kwa Yesu? Kuwa sisi ni safi au sio safi hiyo sio kazi yetu tuliyoitiwa Mungu ndiye atakayesimama kumtetea yule aliyemtuma, achilia haki zako katika mikono ya Mungu aliye hai, ni yeye ndiye atakayeamua kama wewe ni safi au la!  Mungu hajaagiza sisi kujihami, wala kujisafisha  maandiko yanaonyesha ya kuwa sisi tumeitwa kuwa jalala na kufanya kuwa takataka za dunia kuwa kama watu wa kuhukumiwa  Paulo mtume alisema nadhani kuwa sisi tuna wito huu wito wa kutukanwa, wito wa kusingiziwa, wito wa kusemwa vibaya wito wa kuonewa wito wa kuhukumiwa wito wa kuwafanya wenguine wafurahi, wito wa kudharaulika  ona 

1Wakorintho 4:9-13 “Maana nadhani ya kuwa Mungu ametutoa sisi mitume mwisho, kama watu waliohukumiwa wauawe; kwa sababu tumekuwa tamasha kwa dunia; kwa malaika na wanadamu. Sisi tu wapumbavu kwa ajili ya Kristo, lakini ninyi ni wenye akili katika Kristo; sisi tu dhaifu, lakini ninyi mna nguvu; ninyi mna utukufu, lakini sisi hatupati heshima. Hata saa hii ya sasa, tuna njaa na kiu, tu uchi, twapigwa ngumi, tena hatuna makao; kisha twataabika tukifanya kazi kwa mikono yetu wenyewe. Tukitukanwa twabariki, tukiudhiwa twastahimili;tukisingiziwa twasihi; tumefanywa kama takataka za dunia, na tama ya vitu vyote hata sasa.”

Unaona hatupaswi kujipanga kujibu hoja wako watu wanajua kujieleza kuliko sisi nakumbuka wako watu wanao uwezo wa kusema hata uongo ukaonekana kuwa kweli mimi binafsi sina uwezo huo mimi binafsi siwezi kesi mimi nikienda na mtu muongo kwenye kesi yeye atashinda sijazoea vikao vya fujo naweza vikao vya amani siwezi mimi kujitetea naweza kunyamaza kimya hata mbele ya wanaonishutumu na kunichukia hata bila sababu Mungu hakutuagiza kufanya hivyo Mungu ameagiza kulinda mioyo yetu tu

Mithali 4:23 “Linda moyo wako kuliko yote uyalindayo; Maana ndiko zitokako chemchemi za uzima

Swala la mimi ni mzuri au mbaya hiyo sio kazi yangu, mimi ni mwanadamu sijajiumba mwenyewe mwenye mzigo wake aliyeniita akaniokoa akanipa kazi hii ya injili  atajijua mwenyewe kama mimi ni dhaifu sio kazi yangu kuondoa udhaifu wangu ni kazi yake yeye aliyeniita wala sio kazi yangu kuwajibu wale wanaoshutumu kwani inawezekana pia Mungu akawatuma wafanya kazi ya kututukana tunapojaribu kujitetea inawezekana ndio tukaharibu zaidi watuite freemason au waseme lolote wanaloweza kulisema wewe fanya kile ulichoitiwa, kwa sababu kama tuko duniani ukiwanyamazisha hawa hawa watainuka so kazi ya kunyamazisha wanaotushutumu itafanywa na Mungu mwenyewe  ndio mimi ni kondoo tu kati ya wakata manyoya huenda Mungu amewatuma wanitukane hivi ndivyo alivyofanya Daudi wakati wa kushutumiwa kwake ona

2Samuel 16:5-11. “Basi mfalme Daudi alipofika Bahurimu, tazama, kulitoka huko mtu wa jamaa ya nyumba ya Sauli, jina lake akiitwa Shimei, mwana wa Gera; alitoka, akalaani alipokuwa akienda. Tena akamtupia Daudi mawe, na watumishi wote wa mfalme Daudi; na watu wote na mashujaa wote walikuwako mkono wake wa kuume na mkono wake wa kushoto. Na Shimei alipolaani, alisema hivi, Nenda zako! Nenda zako! Ewe mtu wa damu! Ewe mtu usiyefaa!  Bwana amerudisha juu yako damu yote ya nyumba ya Sauli ambaye umetawala badala yake; naye Bwana ametia ufalme katika mkono wa Absalomu mwanao; kisha, angalia, wewe umetwaliwa katika uovu wako mwenyewe, kwa sababu umekuwa mtu wa damu. Ndipo Abishai mwana wa Seruya, akamwambia mfalme, Mbona mbwa mfu huyu amlaani mfalme bwana wangu? Na nivuke, nakusihi, nikaondoe kichwa chake. Mfalme akasema, Nina nini na ninyi, enyi wana wa Seruya? Kwa sababu yeye analaani, na kwa sababu Bwana amemwambia, Mlaani Daudi, basi, ni nani atakayesema, Mbona umetenda haya? Daudi akamwambia Abishai, na watumishi wake wote, Angalieni, huyu mwanangu, aliyetoka viunoni mwangu, anautafuta uhai wangu; si zaidi Mbenyamini huyu sasa? Mwacheni alaani, kwa sababu Bwana ndiye aliyemwagiza.”

Unaiona Daudi alikuwa ni mfalme tena ni askari na alikuwa akizunghukwa ma majemadari wakubwa wa vita alafu anatokea mtu anamtukana hana hata silaha anarusha mavumbi na kumshutumu, Abishai moja ya majemadari wa Daudi akasema huyu ni mbwa mfu anawezaje kumtukana mfalme tunaweza kumshughulikima mara moja Lakini Daudi akasema aaachiwe  Bwana amemtuma afanye hivyo! Oooh inahitaji uvumilivu mkubwa wako watu wametumwa watutukane watusengenye, watushutumu, watulaani, waseme sisi ni waongio, waseme sisi hatufai, waseme uongo na uzushi watupige vijembe, watudhulumu watunyanyase watuseme vibaya kaa kimya hao ni wakata manyoya tu! Wanafanya Pruning ili usipate magonjwa ili usijivune ili uendelee kumtegemea Mungu ili kuonyesha ukomavu wako na ili uweze kuwa na mbele nzuri unahitaji kuvumilia na unahitaji kukaa kimya !    

Kunyamaza mbele ya wakata Manyoya !

Unadhani unaweza kufanya nini kama watu hawakubali kukuelewa? Unadhani unaweza kutatua tatizo? Unadhani unaweza kujibadilisha ukawa kama wanavyotaka? Wamechagua kukuelewa hivyo lazimka ukubali na kuwa mkimyaaa wao hawauhsiki na maisha yako ya baadaye? Wala hawana nguvu ya kuamua hatima yako Mungu haweki hatima yetu katika mikono ya watu wapuuzi, wala mabaradhuri Mungu huweka hatima yetu katika mikono yake yeye ndiye aliyetuumba nan i yeye ndiye mwenye kusudi na sisi  na hakuna mtu anaweza kushindana na kusudi la Mungu na kile ambacho Mungu amekikusudia katika maisha yako hivyo nyamaza mbele ya wakata manyoya kazi yako ni kutimiza wajibu wako na lile kusudi ambalo kwalo Mungu amekuitia haijalishi watu watatuheshimu au watatudharau mwache Mungu afanye yake achana na watu wanaotaka uonekane mbaya pale kazini, shuleni mtaani na katika jamii wakati mwingine hawawezi kuonekana wazuri mpaka wakufanye wewe mzuri kuwa mbaya, wewe endelea na kazi uliyoitiwa, endele kufurahi, endelea kuwa na tabasamu, wao ni wakata manyoya tu, kazi ya kuotesha mengine ni ya Mungu nay ale wanayayafanya ni kwa faida yako kubwa sana , huitaji nguvu kubwa sana kushindana na wanaokupinga nadhani unahitaji nguvu kubwa sana kulinda moyo wako, Mungu anayo njia nzuri sana ya kukusafisha na kukuweka panapo nafasi, Mungu atashughulika mwenyewe wala hataachilia uonevu utamalaki

Zaburi 105:14-15. “Hakumwacha mtu awaonee, Hata wafalme aliwakemea kwa ajili yao. Akisema, Msiwaguse masihi wangu, Wala msiwadhuru nabii zangu.”

Jukumu la kutokuacha au kuachilia tuonewe ni la Mungu mwenyewe, sisi tukae kimya mbele ya wakata manyoya Mungu ndiye atakayetuhesabia haki kwani ni yeye ndiye aliyetufia msalabani, ni yeye aliyeteseka kwa niaba yangu, ni yeye ndiye aliyeninunua kwa damu ya thamani, siwajibiki kwa mtu nawajibika kwa Mungu, sisemi na umbwa nasema na mwenye umbwa amabaye ni Mungu mwenyewe na kwa sababu hiyo tembea kifua mbele, tembea kwa ujasiri asikubughudhi mtu moyo wako aliyetuumba sisi ni Mungu, aliyetuokoa ni Mungu aliyetuita kwenye huduma ni Mungu anayetuelewa ni Mungu na anayetutetea ni Mungu kwa hiyo hakuna sababu ya moyo wako kuinama nyamaza kimya usiwajibu kitu wakata manyoya Mungu ndiye atakaye wajibu.

 

Warumi 8:33-39 “Ni nani atakayewashitaki wateule wa Mungu? Mungu ndiye mwenye kuwahesabia haki. Ni nani atakayewahukumia adhabu? Kristo Yesu ndiye aliyekufa; naam, na zaidi ya hayo, amefufuka katika wafu, naye yuko mkono wa kuume wa Mungu; tena ndiye anayetuombea. Ni nani atakayetutenga na upendo wa Kristo? Je! Ni dhiki au shida, au adha, au njaa, au uchi, au hatari, au upanga? Kama ilivyoandikwa, ya kwamba, Kwa ajili yako tunauawa mchana kutwa, Tumehesabiwa kuwa kama kondoo wa kuchinjwa. Lakini katika mambo hayo yote tunashinda, na zaidi ya kushinda, kwa yeye aliyetupenda. Kwa maana nimekwisha kujua hakika ya kwamba, wala mauti, wala uzima, wala malaika, wala wenye mamlaka, wala yaliyopo, wala yatakayokuwapo, wala wenye uwezo, wala yaliyo juu, wala yaliyo chini, wala kiumbe kinginecho chote hakitaweza kututenga na upendo wa Mungu ulio katika Kristo Yesu Bwana wetu.

Faidha kubwa ya kunyamaza kimya mbele ya wakata manyoya ni kuwa Mungu mwenyewe atafanya kitu cha ziada kama alibyo tabiri Isaya ona

Isaya 53:10-12 “Lakini Bwana aliridhika kumchubua; Amemhuzunisha; Utakapofanya nafsi yake kuwa dhabihu kwa dhambi, Ataona uzao wake, ataishi siku nyingi, Na mapenzi ya Bwana yatafanikiwa mkononi mwake; Ataona mazao ya taabu ya nafsi yake, na kuridhika. Kwa maarifa yake mtumishi wangu mwenye haki Atawafanya wengi kuwa wenye haki; Naye atayachukua maovu yao. Kwa hiyo nitamgawia sehemu pamoja na wakuu, Naye atagawanya nyara pamoja nao walio hodari; Kwa sababu alimwaga nafsi yake hata kufa, Akahesabiwa pamoja na hao wakosao. Walakini alichukua dhambi za watu wengi, Na kuwaombea wakosaji.              

Mungu alimuinua juu Kristo na kumuwadhimisha mno na kumkirimia jina lipitalo majina yote, kazi yetu sio lazima ikubalike na wanadamu kwa sababu sio wao waliotutuma, kazi yetu itathibitishwa na Mungu mwenyewe aliye hai hivyo tunapokutana na changamoto za aina mbalimbali hatuna budi kuhakikisha kuwa tunanyamaza kimya, tusijisafishe, tusilalamike tutulie kimya mbele za Mungu na kuendelea na majukumu yale ambayo Mungu ameyaweka mbele yetu na jitahidi uwe na amani moyoni mwako ukijua wazi ya kuwa Mungu ndiye anayehusika na maisha yetu kwa hali zote

Hakuna mwanadamu alisemwa vinaya kama Yesu, walisema amechanganyikiwa, walimwita ana pepo, walisema anatoa pepo kwa mkuu wa Pepo, Yeye aliendelea kuponya wagonjwa, kuwasaidia wenye shida kulisha wenye njaa na kuwafundisha wenye uhitaji, kwa sababu yako makundi ya watu waliamua kutokumuelewa na yeye aliwaacha, kumbuka Yusufu hakufanya kazi ya kujitetea kuhusu zinaa aliyosingiziwa na mke wa Potifa, kumbuka Nehemia aliendelea na kazi ya kuujenga ukuta pamoja na manenio mabaya kutoka kwa Tobia na Sanbalat na kazi ya Mungu ikakamilika je unadhani Mungu alikuwa hawaoni kina Tobia na Sanbalat? Je unadhani Mungu hangeweza kuwazuia ndugu yangu kama tumechagua maisha haya ya kumtumikia Mungu basi sisi ni kama Kondoo nayeye ndiye Mchungaji mwema na linapokuja swala la Mwenye Kondoo anataka kukata manyoya tutulie kimya mbele ya wakata manyoya!

 

Na Rev. Innocent Samuel Kamote

Mkuu wa wajenzi Mwenye Hekima!

Kufanyiwa nafasi wakati wa shida!



Zaburi 4:1-3 “Ee Mungu wa haki yangu, uniitikie niitapo; Umenifanyizia nafasi wakati wa shida; Unifadhili na kuisikia sala yangu. Enyi wanadamu, hata lini utukufu wangu utafedheheka? Je! Mtapenda ubatili na kutafuta uongo? Bali jueni ya kuwa Bwana amejiteulia mtauwa; Bwana atasikia nimwitapo.”


Utangulizi:

Leo tutachukua Muda kujifunza kwa undani kuhusiana na kifungu hiki cha Zaburi 4:1-3, lakini hususani zaidi maneno Umenifanyizia nafasi wakati wa shida!  Maneno haya ni ya Muhimu sana kwetu kama yalivyokuwa ya muhimu sana wakati wa Mfalme Daudi mwana wa Yese Mbethelehemu alipokuwa akiandika maneno hayo!,  Wanatheolojia wengi sana wanafikiri kuwa huenda zaburi hii iliandikwa wakati wa mgogoro kati ya Daudi na mwanae Absalom, Lakini mimi nadhani kuwa Zaburi hii iliandikwa wakati Daudi alipokoswa koswa kuuawa na Mfalme Sauli kwa kutaka kupigwa mkuki mara kadhaa, hii ni kwa sababu Zaburi hii ni ya mapema zaidi kabla ya mgogoro wa Daudi na kijana wake Kipenzi Absalom! Hata hivyo kabla ya kuangalia kwa undani kifungu hiki ni muhimu kwetu kuligawa somo hili katika vipendele vitatu vifuatavyo:- 


·         Maana ya neno Nafasi

·         Maana ya kufanyiwa nafasi wakati wa shida

·         Kufanyiwa nafasi wakati wa shida 


Maana ya Neno nafasi

Neno nafasi linalotumika hapa lina maana pana sana inayohusiana na swala la kuokolewa katika mazingira magumu, tafasiri nyingi za kimaandiko zimetumika kulielezea neno hili katika maneno ya namna mbalimbali, mfano  King James Version imetumia neno “..Thou hast ENLARGED me when I was in distress” Biblia ya kiingereza ya English Standard Version imetumia neno “…You have given me RELIEF when I was in distress, New Language translation imetumia neno “…Oh God who DECLARE ME INNOCENT, FREE ME from my Troubles”  nyingine ijulikanayo kwa kifupi kama MSG imeandika namna hii “ …God take my side in a tight place” na nyingine imesema “…Free me from affliction  unaona unaposoma matoleo tofauti tofauti ya Biblia mbalimbali inatusaidia kupata maana halisi iliyokusudiwa kwa sababu neno NAFASI lililotumika kwenye Kiswahili linaweza kutunyima uwanja mpana wa kuelewa lile lililokusudiwa lakini kama unajua kiingereza kwa mbali sasa unatkuwa umeanza kufahamu kuwa Daudi alifanyiwa na Mungu tukio kubwa sana la WOKOVU,  Mungu ALIMKUZA baada ya kupitia shida, Mungu alimpa AHUENI baada ya kupitia shida, Mungu alimpa NAFUU baada ya kupitia dhiki, Mungu alimuhesabia HAKI, au KUWA HANA HATIA na kumuweka huru kutoka katika taabu,  unaona neno hilihilo ndilo alilolitumia Isaka alipokuwa akisumbuliwa na Wafilisti kuhusu visima vya baba yake kila alipochimba kisima walipata mgogoro na akwaachia, akachimba kingine wakaleta mgogoro akawaachia hatimaye pale walipoacha kumsumbua ndio akasema Bwana ametupa Nafasi, ahueni,  ona  


Mwanzo 26:18-25 “Isaka akarudi akavichimbua vile visima vya maji walivyovichimba siku za Ibrahimu babaye; maana wale Wafilisti walikuwa wamevifukia baada ya kufa kwake Ibrahimu; naye akaviita majina kufuata majina alivyoviita babaye. Watumwa wa Isaka wakachimba katika lile bonde, wakapata kisima cha maji yanayobubujika. Wachungaji wa Gerari wakagombana na wachungaji wa Isaka wakisema, Maji haya ni yetu. Ndipo akakiita jina la kile kisima Eseki, kwa sababu waligombana naye. Wakachimba kisima kingine, wakagombania na hicho tena. Akakiita jina lake Sitna. Akaondoka huko akachimba kisima kingine, wala hicho hawakukigombania. Akakiita jina lake Rehobothi, akasema, Kwa kuwa sasa BWANA ametufanyia nafasi, nasi tutazidi katika nchi. Akapanda kutoka hapo mpaka Beer-sheba. BWANA akamtokea usiku uleule, akasema, Mimi ni Mungu wa Ibrahimu baba yako, usiogope, maana mimi ni pamoja nawe, nami nitakubarikia, na kuzidisha uzao wako kwa ajili ya Ibrahimu mtumishi wangu.  Akajenga madhabahu huko, akaliitia jina la BWANA. Akapiga hema yake huko, na watumwa wa Isaka wakachimba kisima huko  


unaona Isaka alipata changamoto kutoka kwa maadui zake hakupata nafuu, hakupata auhueni hakupata hata nafasi ya kumuabudu Mungu kwa kumjenge madhabahu maana maisha hayakuwa na utulivu kwa sababu alichukiwa kwa sababu alionewa wivu kwa sababu alifukuzwa kwa sababu waligombana sana sasa anapata kisima ambacho hakikugombewa na hapa anapaita REHOBOTH asili ya neno Nafasi katika lugha ya kiibrania  linakotokea neno REHOBOTH ni “RACHAB” kwa matamshi ni RAW-KHAB  au aliyeshinda changamoto kwa kiarabu RAQEEB.  Kila mwanadamu anahitaji utulivu, anahitaji nafasi, anahitaji usalama anahitaji kushinda changamoto mbalimbali anazokabiliana nazo katikka maisha watu wanaweza kukuchukia pasipo sababu, unaweza kuandamwa hata na watu wenye nguvu sana, matajiri kuliko wewe, wenye mali kuliko wewe unaweza kuhisi uonevu kila mahali, unaweza kuionewa na kutafutwa na adui zako, magonjwa mateso, dhuluma bna changamoto za aina mbalimbali na unahitaji ufikie nafasi ambayo Mungu atakupa ahueni, atakupa nafasi, atakuondolea mashaka atakupa kuponyoka katika mikono ya adui hii ndio nafasi kwa ujumla inazungumzia wokovu katika kifurushi chake kamili tunahitaji nafasi! 

Maana ya kufanyiwa nafasi katika shida! 

Zaburi 4:1-3 “Ee Mungu wa haki yangu, uniitikie niitapo; Umenifanyizia nafasi wakati wa shida; Unifadhili na kuisikia sala yangu. Enyi wanadamu, hata lini utukufu wangu utafedheheka? Je! Mtapenda ubatili na kutafuta uongo? Bali jueni ya kuwa Bwana amejiteulia mtauwa; Bwana atasikia nimwitapo.” 

Baada ya uchambuzi wa kina hapo juu kuhusu kufanyiwa nafasi, nadhani sasa unaweza kuelewa vema zaburi hii kuwa mtumishi wa Mungu Daudi alikuwa anapitia changamoto ya aina gani, narudia tena kusema wazi kuwa changamotio yake haikuwa wakati wa Absalom bali ni wazi kabisa ukiangalia maana ya chimbuko la Neno nafasi Daudi anayodai kufanyiwa na bwana ni wazi kuwa Daudi hapa anakumbuka nanma alivyoponyoka katika mikono ya Sauli, wakati wa vita na Absalom Daudi alikuwa ni Mfalme hivyo tayari alikuwa ana nafasi, alikuwa na majemadari wajuzi wa vita na wapelelezi wa kutosha pamoja na kuwa moyo wake ulibaki ukimtegema Mungu, Lakini wakati huu alikuwa mpiga kinubi tu, alikuwa masikini bado alikuwa akijifunza maswala ya utawala alikuwa mnyonge na eti mfalme anataka kumuua kwa kumpiga mkuki maandiko yanatuonyesha kuwa sio mara moja wala sio mara mbili na katika matukio yote hayo Mungu aliingilia kati 

1Samuel 18:9-14 “Sauli akamwonea Daudi wivu tangu siku ile. Ikawa siku ya pili yake, roho mbaya kutoka kwa Mungu ikamjilia Sauli kwa nguvu, naye akatabiri ndani ya nyumba. Basi Daudi alikuwa akipiga kinubi kwa mkono wake kama siku zote; naye Sauli alikuwa na mkuki mkononi mwake.  Mara Sauli akautupa ule mkuki; maana alisema, Nitampiga Daudi hata ukutani. Daudi akaepa, akatoka mbele yake, mara mbili. Sauli akamwogopa Daudi, kwa sababu Bwana alikuwa pamoja naye, ila amemwacha Sauli. Kwa ajili ya hayo Sauli akamwondosha kwake, akamfanya awe akida wake juu ya askari elfu; naye akatoka na kuingia mbele ya watu. Naye Daudi akatenda kwa busara katika njia zake zote naye Bwana alikuwa pamoja naye.” 

1Samuel 19: 10-12 “Sauli akajaribu kumpiga Daudi hata ukutani kwa mkuki wake, ila yeye akaponyoka kutoka mbele ya Sauli, nao huo mkuki akaupiga ukutani; naye Daudi akakimbia, akaokoka usiku ule. Kisha Sauli akatuma wajumbe mpaka nyumbani kwa Daudi, ili wamvizie na kumwua asubuhi; naye Mikali, mkewe Daudi, akamwambia, akasema, Wewe usipojiponya nafsi yako usiku huu, kesho utauawa. Basi Mikali akamtelemsha Daudi dirishani; naye akaenda akakimbia na kuokoka.” 

Ni ukweli ulio wazi kabisa kuwa ukiangalia asili ya kuchomoka kwa Daudi katika mikono ya Sauli ilifanywa na Mungu mwenyewe haikuwa akili ya Daudi,  ni mpaka Adui wa daudi walitambua ya kuwa Mungu yuko Pamoja naye, unajua kuna wakati watu wanaweza kukutafuta waklufanyie mabaya wanaweza kukusudia  mabaya dhidi yako, lakini kila wanapopanga mbinu zao na mikakati yao wanakuja kugundua kuwa unateleza kama samaki mbichi Mungu anakulinda na kukuepusha na kila kitu kibaya mpaka wanagundua ya kuwa Mungu yu Pamoja nawe!, umeona Adui wa Isaka walimfuata eee mwisho waalipogundua kuwa kila wakimdhulumu Bwana anamfanyia nafasi wakagundua kuwa Bwana yuko pamoja naye , na sauli vilevile alimuogopa Daudi kwa sababu alijua kuwa Bwana yuko pamoja naye 

Mwanzo 26: 26-30 “Ndipo Abimeleki akamwendea kutoka Gerari, pamoja na Ahuzathi rafiki yake, na Fikoli, jemadari wa jeshi lake. Isaka akawauliza, Mbona mwanijia, nanyi mmenichukia, mkanifukuza kwenu? Wakasema, Hakika tuliona ya kwamba BWANA alikuwa pamoja nawe; nasi tukasema, Na tuapiane, sisi na wewe, na kufanya mapatano nawe  ya kuwa hutatutenda mabaya, iwapo sisi hatukukugusa wewe, wala hatukukutendea ila mema, tukakuacha uende zako kwa amani; nawe sasa u mbarikiwa wa BWANA.  Basi akawafanyia karamu, nao wakala, wakanywa.” 

Unaona Mungu anapokufanyia nafasi anakupoa utulivu, anakubariki, anakupa amani, anakupatanisha na adui zako, anakupa kibali lakini ili nafasi iweze kupatikana ni lazima shida ziwepo, hatupendi kupita katika shida na mateso ya aina mbalimbali lakini Mungu huwa anaziruhusu kwa makusudi na mapenzi yake mema ili ziweze kutuinua na kuzalisha kitu kingine cha ziada katika maisha yetu 

Kufanyiwa nafasi wakati wa shida 

Ni muhimu kuwa na ufahamu wa kutosha kuwa kila changamoto unayoipitia haimaanishi kuwa Munghu hajajibu maombi yako, haimaanishi kuwa Mungu anakuhukumu kwa sababu umefanya dhambi, haimaanishi kuwa Munu hakujali lakini vyovyote ilivyo Mungu ndiye haki yetu, Na amemfanya Yesu Kristo kuwa haki yetu sisi hatuna haki yetu wenyewe, Lakini sio hivyo tu yeye ndiye Mwokozi nan i yeye ndiye mwenye haki ya kutuhukumu na sio mtu mwingine, unaweza kuwa unapitia changamoto, za aina mbalimbali na ukadhani kuwa umerogwa au Mungu amechukizwa naye au hayuko pamoja nawe inaweza kuwa una taabu kubwa sana zinakusonga adui mkubwa mara tatu zaidi yako, unatafutwa kuuawa, unajiona una nuksi, unajina una balaa, unajiona hufanikiwi unajiona umechelewa unaweza kuchoka na kujiuliza nini kinanitokea katika maisha yangu wengine wanaweza kudhani labda wameoa mwanamke mwenye mikosi au mwameolewa na abila lenye mikosi au balaa na unaweza kujiuliza maswala nini kinaendelea katika maisha yangu lakini dhiki zetu ni nafasi ni opportunity, Mungu anatupa  Nafasi itakayotupeleka katika ngazi nyingine na kutuinua, kutupa ahueni, kutupa nafuu, kutupa tahafifu, kutuponya kutuweka huru, kututangaza kuwa hatuna hatia kutupa raqeeb kutuweka panapo nafasi 

1Wakoritho 10:13 “Jaribu halikuwapata ninyi, isipokuwa lililo kawaida ya wanadamu; ila Mungu ni mwaminifu; ambaye hatawaacha mjaribiwe kupita mwezavyo; lakini pamoja na lile jaribu atafanya na mlango wa kutokea, ili mweze kustahimili.” 

Daudi alivumilia na kuliitia jina la Bwana katika dua zake na hatimaye Mungu alimpa upenyo, Leo nakutangazia na ninakutabiaria na ninatamka na kuzushuhudia mbingu na ardhi na kuziap[iza kwa jina la Yesu Kristo ya kwamba changamoto zako unazozipitia na shida unazipitia zikuletee mafanikio, zikuleteee amani na furaha, zikuletee Baraka, zikuletee tumaini, zikuletee nafuu, zikuleteee kibali, zikuletee ahueni, zikuletee uponyaji, zimletee Mungu utukufu, zikuletee kutoboa zikupatanishe na adui zako kumbuka kila wakati upitiapo shida kuna nafasi nasema kuna nafasi na Mungu ni mwaminifu! Utachanua katika jina la Yesu Kristo mwana wa Mungu aliye hai!

 

Rev. Innocent Samuel Kamote

Mkuu wa wajenzi mwenye Hekima!

Jumatatu, 20 Februari 2023

Ikawa Mwanzo wa Mwaka Mpya!


2Samuel 11:1-4 “Hata ikawa, mwanzo wa mwaka mpya, wakati watokapo wafalme kwenda vitani, Daudi akampeleka Yoabu, na watumishi wake pamoja naye, na Israeli wote; wakawaangamiza wana wa Amoni, wakauhusuru Raba. Lakini Daudi mwenyewe akakaa Yerusalemu. Ikawa wakati wa jioni, Daudi akaondoka kitandani, akatembea juu ya dari ya jumba la mfalme; na alipokuwa juu ya dari aliona mwanamke anaoga; naye huyo mwanamke alikuwa mzuri sana, wa kupendeza macho. Naye Daudi akapeleka, akauliza habari za yule mwanamke. Mtu mmoja akasema, Je! Huyu siye Bath-sheba, binti Eliamu, mkewe Uria, Mhiti? Basi Daudi akapeleka wajumbe, akamtwaa; naye akaingia kwake; naye akalala naye; (maana yule mwanamke amekwisha kutakasika unajisi wake); kisha akarudi nyumbani kwake.



Utangulizi:

Ni muhimu kufahamu kuwa kifungu hiki cha maandiko kina jambo kubwa la msingi la kutufundisha ambalo mwandishi wa kifungu hiki alikuwa anakusudia kukileta kwetu! Wengi wetu tunafahamu sana habari ya anguko la Daudi katika zinaa, na tunafahamu madhara makubwa yaliyompata kutokana na dhambi hii, lakini vilevile tunaweza kukubaliana wazi kuwa Daudi alikuwa na udhaifu sawa na ule walionao wanaume wengine, kwamba aliona mwanamke mzuri anaoga akamtamani, na kuzini naye na wengi wameweza kumalumu Daudi kwa sababu mbalimbali hata ikiwa ni pamoja na kujenga Ghorofa lenye dari ya kutembelea na kusababisha kuona mke wa jirani yake ambaye alikuwa anaoga, tunaweza kuwa na sababu lukuki kuhusu anguko la Mfalme Daudi na sababu hizo zikawa na mashiko kadhaa, Lakini mwandishi wa kifungu hiki ana sababu mojawapo ya muhimu zaidi ambayo kimsingi ndio nataka tuiangalie kwa kina katika siku kama hii ya leo!

Ikawa Mwanzo wa Mwaka mpya!

Mwandishi anaanza kwa kueleza Habari ya anguko la Daudi akiwa na sababu nyingine tofauti mno Ikawa Mwanzo wa Mwaka Mpya! Wakati watokapo wafalme kwenda vitani!  Majira ya nchi katika mashariki ya kati yanafanana sana kwa kiwango kikubwa na majira ya Afrika ya mashariki, Mwezi wa Januari na February Mpaka March ndio miezi ambayo tunaweza kuyaita majira ya Mwanzo wa mwaka kunakuwa na Joto kali na ukavu wa aina Fulani, katika majira haya kwa wana wa Israel huangukia kati ya mwezi wa Abibu au mwezi (Nisani) katika majira haya ardhi huwa kame na kavu, na hivyo ndio majira ambayo wafalme wengi waliyatumia kuingia vitani kwa kusudi la kupanua mipaka ya mataifa yao, kuteka nyara, kulipisha kodi wale utakaowashinda au kulinda mipaka yako, wakati huu ulikuwa ni wakati muafaka kwa vita kwa sababu ardhi ilikuwa kavu, na hivyo iliweza kurahisisha vita vya miguu, magari ya kukokotwa na farasi lakini pia kusafirisha silaha na wanajeshi kwa urahisi zaidi kuliko wakati wa baridi na wakati wa mvua ambapo ardhi huwa na matope na vita vinakuwa ni ngumu,  wakati huu pia ilikuwa ni rahisi kuteka nyara vitu na kuvibeba kwa hiyo ilikuwa ni desturi ya Wafalme kutoka kwenda kupigana vita mwanzoni mwa mwaka mpya, Hata Mungu aliwaokoa wana wa Israel kutoka Misri katika majira kama haya.

Kutoka 12;1-2”BWANA akanena na Musa na Haruni katika nchi ya Misri, akawaambia, Mwezi huu utakuwa mwanzo wa miezi kwenu; utakuwa ni mwezi wa kwanza wa mwaka kwenu”.

Kwa hiyo wataalamu wa nyakati waliweza kuuelewa vema kuwa ulikuwa ni wakati gani na wanapaswa kufanya nini, Mwandishi anataka kutuonyesha kuwa Sababu zilizopelekea Daudi kufanya dhambi au kuanguka dhambini ilikuwa ni  pamoja na:-

1.       Aliudharau wakati – kumbe ilikuwa wazi kabisa na ilikuwa inajulikana kabisa kwamba Mwanzo wa mwaka mpya ni lazima wafalme watoke kwenda kupigana vita, Lakini yeye aliupuuzia wakati  Moja ya tatizo kubwa linaloweza kumleta mwanadamu katika anguko la maisha yake ni kutokujua kuutumia wakati, kuna madhara mengi na majuti makubwa sana kwa kila mwanadamu ambaye hakujua kuutumia wakati, wakati tuliopewa duniani ni mfupi sana na unaenda haraka mno, wastaafu wengi wanajua leo kwa sababu hawakujua kuutumia wakati, vijana wengi wanafikiri wataendelea kuwa vijana tu, wasichana wengi wanadhani wataendelea kuwa wasichana tu, wanafunzi wengi sana wanadhani iko siku watakaa ajipange na kusoma kwa bidii na sasa wengi wanalala na kupoteza muda wakifikiri uko wakati, Hakuna jambo linaumiza sana kama kuja kugundua baadaye kuwa sikuutumia wakati, nilikuwa wapi mimi? Hakuna jambo linaumiza kama kupotezewa wakati!  Kila mmoja wetu anapaswa kufahamu kuwa wakati usipoutumia vema anguko lake ni kubwa  na lenye kuleta madhara makubwa sana duniani, kwa hiyo ni vema kuutumia wakati na kutokuupuuza Yesu alilalamika kwa njia ya kinabii kwa mji wa Yerusalem kwamba utabomolewa na kuharibiwa vibaya sana na Majeshi ya warumi tukio ambalo lilitimizwa mwaka wa 70 baada ya Kristo lakini malalamiko ya Yesu kwa Yerusalem ni kwa sababu tu ya kutokuujua majira na wakati hususani Mwokozi wa ulimwengu alipowatembelea.

 

Luka 19:41-44 “Alipofika karibu aliuona mji, akaulilia, akisema, Laiti ungalijua, hata wewe katika siku hii, yapasayo amani! Lakini sasa yamefichwa machoni pako. Kwa kuwa siku zitakuja, adui zako watakapokujengea boma, likuzunguke; watakuzingira na kukuhusuru pande zote; watakuangusha chini wewe na watoto wako ndani yako, wasikuachie jiwe juu ya jiwe, kwa sababu hukutambua majira ya kujiliwa kwako.”

 

Daudi alifahamu wazi kuwa ulikuwa ni wakati wa wafalme kwenda vitani lakini yeye hakwenda vitani, alibaki anarandaranda mjini tu na hiki ndio moja ya sababu ambayo mwandishi anaiona kuwa Daud alikosea!

 

2.       Aliudharau wajibu -  Kupigania watu ulikuwa ni moja ya wajibu wa waamuzi na wafalme Daudi alikuwa anawajibika kabisa kwenda vitani, huu ulikuwa ni wajibu wake na wajibu wa wafalme wa mataifa yote, ndio kuna wakati unaweza kumtuma mtu aende, Lakini mwandishi anaonyesha kuwa tatizo hapa lililopelekea habari kuwa nyingine kwa Mfalme Daudi ni kutokwenda vitani yeye alimtuma Yoabu aende, wakati mwingine ili Mungu aweze kuleta ukombozi kwa jamii ni lazima waweko watu watakaokubali kubeba wajibu, kama kila mmoja wetu akibeba wajibu wake kwa ufanisi tutaweza kuona mwanga

 

Luka 1:38 “Mariamu akasema, Tazama, mimi ni mjakazi wa Bwana; na iwe kwangu kama ulivyosema. Kisha malaika akaondoka akaenda zake.”

 

Mariam alikubali kuubeba wajibu wa kumzaa Yesu na akaleta faida Kubwa sana Duniani, walimu wakifanya wajibu wao, wanafunzi wakifanya wajibu wao, wanasiasa wakifanya wajibu wao na  wananchi wakifanya wajibu wao hakuna kitakachoshindikana, mke naye afanye wajibu wake na mume naye afanya wajibu wake kila mmoja atimize wajibu, wake kila mmoja akitimiza wajibu wake hakuna changamoto itakayojitokeza popote, Daudi alikwepa wajibu, na kudharau muda na majira aliyotakiwa kwenda vitani na matokeo yake alipatwa na anguko la kihistoria, hatuwezi kumlaumu yeye kwa sababu zozote zile kwani kuna kitu cha kujifunza kutoka kwake lakini mwandishi anatuonyesha kuwa moja ya sababu ya anguko lake ni kudharau wajibu, inapotokea kuwa shetani akatutia katika kishawishi cha kutokuzingatia kutimiza wajibu tunaweza kujikuta tunajutia maisha yetu yote na kusema laiti ningelijua kwa msingi huo ni muhimu kwetu tukatimiza wajibu, najua ziko ndoa nyingi sana zinapitia kwenye changamoto ambazo kimsingi ni kwa sababu tu watu hawataki kutimiza wajibu wao, kila mmoja akimfanyia mwenziwake kile ambacho maandiko yameagiza basi, katika jamii yetu kama kila mmoja wetu atatimiza wajibu kamwe haitakuja tuone madhara na majuto baadaye timiza wajibu.

 

3.       Kupenda rahisi/au uvivu – kupenda rahisi au uvivu kuna madhara makubwa sana katika maisha yetu tunaambiwa kuwa Daudi alikaa tu onaLakini Daudi mwenyewe akakaa Yerusalemu.”Maana yake alikaa tu hakufanya kazi, Daudi aliingiwa na uvivu, mtu akikaa tu bila jambo la Muhimu la kufanya, kinachofuata sasa ni kumpa ibilisi nafasi, “Idlenes gives great adavantage to the temper  Neno la Mungu linapingana vikali sana na swala zima la la uvivu, na wakati wote neno la Mungu linatutaka kupingana na tatizo la uvuvi na linawataka watu wafanye kazi likiwa na mifano mingi sana na maelekezo mengi sana mfano

 

Mithali 6:6-11 “Ewe mvivu, mwendee chungu, Zitafakari njia zake ukapate hekima. Kwa maana yeye hana akida, Wala msimamizi, wala mkuu, Lakini hujiwekea akiba ya chakula wakati wa jua; Hukusanya chakula chake wakati wa mavuno. Ewe mvivu, utalala hata lini? Utaondoka lini katika usingizi wako? Bado kulala kidogo, kusinzia kidogo, Bado kukunja mikono upate usingizi! Hivyo umaskini wako huja kama mnyang'anyi, Na uhitaji wako kama mtu mwenye silaha.”

 

Biblia ina la kusema kuhusu uvivu. Kitabu cha Mithali imejawa na hekima kuhusu uvivu na onyo kwa mtu mvivu. Mithali inatuambia kwamba mtu mvivu anachukia kazi:

 

Mithali 21:25 "Matakwa yake mtu mvivu humfisha, kwa maana mikono yake hukataa kufanya kazi."

 

Mithali 26:13-14 “Mtu mvivu husema, Simba yuko njiani, Simba yuko katika njia kuu. Kama vile mlango ugeukavyo katika bawaba zake; Kadhalika mtu mvivu katika kitanda chake.“

 

Mithali 18:9 Yeye naye aliye mvivu katika kazi yake, Ni ndugu yake aliye mharabu. Newton's first law states that, “if a body is at rest or moving at a constant speed in a straight line, it will remain at rest or keep moving in a straight line at constant speed unless it is acted upon by a force”. Mwandishi anaonyesha kuwa taabu nyingine ambayo Daudi ilimpelekea kuingia katika hali hii nzito ya anguko ni kukaa tu bila kufanya shughuli 2 Wathesalonike 3:10 “Kwa kuwa hata wakati ule tulipokuwapo kwenu tuliwaagiza neno hili, kwamba ikiwa mtu hataki kufanya kazi, basi, asile chakula”. Kila mmoja wetu anapaswa kuhakikisha kuwa hatumpi ibilisi nafasi, kila mmoja ahakikishe kuwa anaukomboa wakati na hapotezi muda, muda sio wa kuchezea muda ni mali, lakini wakati huo huo kila mmoja atimize wajibu wake na mwisho tuhakikishe kuwa tunapiga vita uvizu, maswala haya yalipodharauliwa na daudi yalileta anguko kwake ashukuriwe Mungu yeye alianguka katika zinaa lakini anguko baya kuliko yote ni kushindwa maisha hili linaleta majuto makubwa na machungu sana Duniani kuliko naguko la iana nyinguine lolote tunaweza kujiokoa kwa kujituma kwa bidii kwa kutumia nafasi na vipawa tulivyopewa na Mungu na kukamilisha kusudi la Mungu alilolikusudia kwetu Duniani, Neema ya Mungu na ikufunike ikiwa unataka kuishi kama Mfalme katika wakati ujao ni vema ukiyazingatia hayo!

Rev. Innocent Samuel Kamote.

Mkuu wa wajenzi mwenye Hekima!

Waoga katika ziwa liwakalo Moto!


Ufunuo 21:7-8 “Yeye ashindaye atayarithi haya, nami nitakuwa Mungu wake, naye atakuwa mwanangu. Bali waoga, na wasioamini, na wachukizao, na wauaji, na wazinzi, na wachawi, na hao waabuduo sanamu, na waongo wote, sehemu yao ni katika lile ziwa liwakalo moto na kiberiti. Hii ndiyo mauti ya pili.”




Utangulizi:

Ni muhimu kufahamu kuwa moja ya tabia ambayo inawakosesha watu wengi sana Baraka za kiungu ni Pamoja na tabia ya kuwa na WOGA, Mungu ameuweka woga kama moja wapo ya dhambi ya kwanza katika orodha ya watu watakaotupwa katika ziwa la Moto kutokana na kukosa ushindi wa kuingia Mbinguni, kama tunavyoweza kuona katika mstari wa Msingi

Ufunuo 21:7-8 “Yeye ashindaye atayarithi haya, nami nitakuwa Mungu wake, naye atakuwa mwanangu. Bali waoga, na wasioamini, na wachukizao, na wauaji, na wazinzi, na wachawi, na hao waabuduo sanamu, na waongo wote, sehemu yao ni katika lile ziwa liwakalo moto na kiberiti. Hii ndiyo mauti ya pili.”

Ni aina gani ya woga inazungumzwa hapo?  Katika Biblia ya kiingereza ya New international Version neno waoga linasomeka kama COWARDLY  au katika Matoleo mengine ya Biblia kama KJV neno linasomeka kama FEARFUL kwa mujibu wa Lugha ya asili iliyotumika kuandikia agano jipya neno la kiyunani linalotumika hapo ni DEILOS kimatamshi DILOS au DEOS maana yeke ni TIMID  ambalo tunaweza kulitafasiri kwa kiingereza kama a Person who is lacking Courage, au a person who lacks endure  dangerous au a person who fear unpleasant things kwa lugha yetu tunaweza kusema Mwoga ni mtu asiye na ujasiri, au mtu asiyeweza kuvumilia mambo magumu, au anayeogopa hatari, au kuogopa mambo yasiyopendeza au ya aibu,  watu wa aina hiyo utaweza kuona kuwa katika maandiko Mungu hakupenda kuwatumia, watu wa Mungu ni kama askari  na kila mara Mungu anapotuita katika ushirika nayeye huwa anatuagiza kwamba tusiogope, Mungu anajua namna ambavyo woga ni adui mkubwa sana na urithi wetu, woga ni adui wa maendeleo, watu wenye hofu huwa hawafanikiwi sio tu katika maisha haya lakini hata Mbinguni ni vigumu kuingia kama u mwoga!

Nyakati za Biblia Mungu alipowaita watu vitani alihakikisha kuwa waoga wote wanaondolewa kwenye orodha ya wapiganaji na waliobaki walikuwa ni wale waliokuwa na moyo wa ujasiri tu, na haikupaswa wao kuogopa chochote zaidi ya kuku mbuka tu kuwa Bwana yuko pamoja nao, ilikuwa ni lazima kila mwenye sababu zinazoonyesha kuwa hafai kwenda vitani aondolewe na wale waliokwenda walitiwa moyo na kuhani na kuelekea vitani wakiwa wana muamini Mungu tu ona

Kumbukumbu la Torati 20:1-9 “Utokapo kwenda vitani kupigana na adui zako, na kuona farasi, na magari, na watu wengi kuliko wewe, usiwaogope; kwa kuwa Bwana Mungu wako, yu pamoja nawe, aliyekukweza kutoka nchi ya Misri. Na iwe, msongeapo mapiganoni, kuhani na akaribie na kusema na watu, awaambie, Sikizeni, enyi Israeli, hivi leo mwasongea mapiganoni juu ya adui zenu mioyo yenu na isizime; msiche, wala msiteteme, wala msiingiwe na hofu kwa ajili ya wao;  kwa maana Bwana, Mungu wenu, ndiye awaandamaye kwenda kuwapigania juu ya adui zenu, ili kuwaokoa ninyi. Na maakida na waseme na watu, na kuwaambia, Ni mtu gani aliye hapa aliyejenga nyumba mpya, wala hajaiweka wakfu? Aende akarudi nyumbani kwake, asije akafa mapiganoni, ikawekwa wakfu na mtu mwingine. Ni mtu gani aliye hapa aliyepanda shamba la mizabibu, wala hajatumia matunda yake? Aende akarudi nyumbani kwake asije akafa mapiganoni, yakatumiwa na mtu mwingine matunda yake. Ni mtu gani aliye hapa aliyemposa mke wala hajaoa? Aende akarudi nyumbani kwake asije akafa mapiganoni, huyo mwanamke akaolewa na mume mwingine. Tena maakida na waseme zaidi na watu, wawaambie, Ni mtu gani aliye hapa tena mwenye hofu na moyo mnyonge? Aende akarudi nyumbani kwake, isije mioyo ya nduguze ikayeyuka mfano wa moyo wake. Itakuwa hapo watakapokwisha wale maakida kusema na watu, na waweke majemadari wa majeshi juu ya watu.”

Mungu wakati wote aliwataka watu wake wawe na moyo wa ushujaa ona katika Yoshua 1:5-9 “Hapatakuwa mtu ye yote atakayeweza kusimama mbele yako siku zote za maisha yako; kama nilivyokuwa pamoja na Musa, ndivyo nitakavyokuwa pamoja na wewe; sitakupungukia wala sitakuacha. Uwe hodari na moyo wa ushujaa, maana ni wewe utakayewarithisha watu hawa nchi hii niliyowaapia baba zao ya kwamba nitawapa. Uwe hodari tu na ushujaa mwingi, uangalie kutenda sawasawa na sheria yote aliyokuamuru Musa mtumishi wangu; usiiache, kwenda mkono wa kuume, au wa kushoto, upate kufanikiwa sana kila uendako. Kitabu hiki cha torati kisiondoke kinywani mwako, bali yatafakari maneno yake mchana na usiku, upate kuangalia kutenda sawasawa na maneno yote yaliyoandikwa humo; maana ndipo utakapoifanikisha njia yako, kisha ndipo utakapositawi sana. Je! Si mimi niliyekuamuru? Uwe hodari na moyo wa ushujaa; usiogope wala usifadhaike; kwa kuwa Bwana, Mungu wako, yu pamoja nawe kila uendako.”   

Yesu Kristo vile vile anawataka watu wake wawe na ujasiri na ndio maana wakati wote aliwataka wanafunzi wake wawe watu wenye kujikana nafsi lakini vilevile hakutupoa roho ya woga  ona


Luka 9:23-25 “Akawaambia wote, Mtu ye yote akitaka kunifuata, na ajikane mwenyewe, ajitwike msalaba wake kila siku, anifuate. Kwa kuwa mtu atakaye kuiponya nafsi yake ataiangamiza, na mtu atakayeiangamiza nafsi yake kwa ajili yangu ndiye atakayeisalimisha. Kwa kuwa yamfaa nini mtu kuupata ulimwengu wote, kama akijiangamiza, au kujipoteza mwenyewe?


Unaona wanajeshi wakati wote huwa hawayahesabu maisha yaio kuwa kitu, wanapokwenda vitani wanajua kuwa wako tayari kuyatoa maisha yao kwaajili ya taifa lao au kwaajili ya ndugu zao wanajua wazi kuwa unapokwenda vitani kuna kufa na kupona hivyo husimama kidete wakijionyesha kuwa wanaume, Kristo anataka kila mtu anayemfuata kuubeba msalaba wake na kumfuata kila siku, ziko changamoto za kila siku katika maisha yetu zinazohitaji imani yetu kwa Mungu na kwa msingi huo kamwe hatupaswi kuogopa ndio maana Mungu ametupa Roho Mtakatifu ili tuweze kukabiliana na hofu ya maisha haya ona


2Timotheo 1:7-9 “Maana Mungu hakutupa roho ya woga, bali ya nguvu na ya upendo na ya moyo wa kiasi. Basi usiuonee haya ushuhuda wa Bwana wetu, wala usinionee haya mimi mfungwa wake, bali uvumilie mabaya pamoja nami kwa ajili ya Injili, kwa kadiri ya nguvu ya Mungu; ambaye alituokoa akatuita kwa mwito mtakatifu, si kwa kadiri ya matendo yetu sisi, bali kwa kadiri ya makusudi yake yeye na neema yake. Neema hiyo tulipewa katika Kristo Yesu tangu milele,”


Wakati wote ushindi wetu unapatikana kwa njia ya imani katika Mungu, kwa hiyo pasipo imani haiwezekani kumpendeza Mungu, hatuna budi kuhakikisha kuwa tunamwamini Mungu kiasi kwamba tunamtegema yeye kiasi kwamba hatuogopi hatari ya aina yoyote, watu wanaoogopa aibu hawawezi kufanya biashara yenye mtaji mdogo, watu wanaoogopa mitihani wanaweza kufeli hata kama mitihani hiyo ni myepesi, woga unaweza kutukosesha ushindi, 

Nyakati za ikanisa la kwanza  wakati Yohana anaandika kitabu cha ufunuo ulikuwa ni wakati ambapo watu wanaomwamini Yesu kristo walikuwa wanauawa kwa kukatwa na misumeno, kwa kuchimwa moto kama mishumaa baada ya kumwagiwa lami, kwa kukatwa kiungo kimoja kimoja, kwa kuchunwa ngozi huku wakiwa hai, kwa kufunguliwa simba wenye njaa, kwa kusulubiwa na kutundikwa misalabani, kuuawa kwa mikuki na mambo mengine ulikuwa ni wakati mbaya na w mateso ya hali ya juu, katika wakati huu watu wengine walimkana Yesu na kuachiwa huru kwa sababu ndio lilikuwa sharti kubwa ukimkana Yesu unaachiwa huru, kwa hiyo kila Mkristo alipaswa kukubali kukabiliana na kila aina ya mateso atakayokutana nayo na kuvumilia kila hatari utakayokutana nayo na kufa kwaajili ya Kristo ilikuwa ni alama ya ushindi,  wale waliomkana Yesu kutakana na mitihani waliyokutana nayo waliitwa waoga na hawa waliwekwa katika orodha ya kwanza ya watu watakaotupwa katika ziwa la Moto! Kwa nini kwa sababu walimkana Yesu na kuihesabu damu aliyoimwaga kama kitu cha hovyo, wako watu wanaogopa kumkiri Yesu hadharani, wako watu wanamkataa Yesu kwa sababu ndugu zao baba zao na mama zao ni wa imani nyingine neno la Mungu linasema waoga wote sehemu yao ni katika ziwa liwakalo moto, Heri leo umkubali Yesu, heri leo upokee roho ya nguvu ya ujasiri na ya upendo, heri leo ukatae mashetani na mkizimu na majini na mapepo, heri leo ukiri Yesu katika njia zako zote! 

Woga wako ndio kizuizi cha muujiza wako!

Na Rev. Innocent Samuel Kamote

Mkuu wa wajenzi mwenye Hekima