Jumapili, 26 Novemba 2023

Umuhimu wa kufanya Uinjilisti:


Mathayo 28:18-20 “Yesu akaja kwao, akasema nao, akawaambia, Nimepewa mamlaka yote mbinguni na duniani. Basi, enendeni, mkawafanye mataifa yote kuwa wanafunzi, mkiwabatiza kwa jina la Baba, na Mwana, na Roho Mtakatifu; na kuwafundisha kuyashika yote niliyowaamuru ninyi; na tazama, mimi nipo pamoja nanyi siku zote, hata ukamilifu wa dahari.”              




Utangulizi:

Ni muhimu kujikumbusha kwamba moja ya agizo muhimu sana kwa wakristo wote duniani kutoka kwa Bwana wetu Yesu Kristo ni kuhakikisha kuwa watu wote duniani wanaisikia habari njema yaani injili, watu wengi sana huwa wanajisahaulisha kuhusu jambo hili la Muhimu, nimetumia miaka mingi sana kuwatia moyo, na kuwajenga kiimani na kuwafunulia neno la Mungu kama Mwalimu wa neno lake, lakini nitakuwa mchoyo wa fadhila kama nitasahau kukazia jambo hili  la Muhimu, najua kazi niliyokuwa nikiifanya ni sehemu ya injili lakini nasukumwa sana kuzungumzia injili kwa sababu kuna maonyo ya kimaandiko kwetu endapo tutaacha kusema kuhusu habari njema, kwa sababu ni sharti yaani ni lazima kuihubiri injili

1Wakorintho 9:16-17 “Maana, ijapokuwa naihubiri Injili, sina la kujisifia; maana nimewekewa sharti; tena ole wangu nisipoihubiri Injili! Maana nikiitenda kazi hii kwa hiari yangu nina thawabu; ila ikiwa si kwa hiari yangu, nimeaminiwa uwakili.”

Kazi ya kuhubiri injili imetoka katika agizo la kiongozi mkubwa zaidi Duniani na ni kazi ya Muhimu, kanisa yaani watu wa Mungu hawapaswi kwa namna yoyote kupuuzia agizo lake, pamoja na kuwajibishwa kwa watu wasiohubiri injili, lakini kuna madhara makubwa sana kwa ulimwengu kuharibiwa na kazi za shetani, mmomonyoko wa uadilifu, kukosa Nuru, kukosa chumvi, na kuingiliwa kwa ulimwengu na falsafa za giza zilizo kinyume na injili zitaenea na kuifanya dunia kuingia gizani kinyume kabisa na namna Yesu anavyotutarajia tufanye! Endapo tuntutapuuzia swala la kuihubiri injili,  Kwa hiyo tuna wajibu wa kuihubiri injili na hii ni kazi  ya kila muungwana aliyeamini  duniani!

Tutajifunza somo hili umuhimu wa kuihubiri injili kwa kuzingatia vipengele vinne  muhimu vifuatavyo:-

·         Maana ya neno injili.

·         Umuhimu wa kufanya uinjilisti.

·         Madhara ya kuacha kuhubiri injili.

·         Namna nyepesi ya kuifikisha injili


Maana ya neno Injili.

Neno injili limetokana na neno la kiingereza Evangelism ambalo kwa kiyunani ni EUANGELIUM  na kwa kilatini ni GOSPEL ambalo maana yake (Good Story) au (Good News)kwa Kiswahili Habari njema, au kuwaeleza watu habari nzuri, habari za matumaini au habari za kutia moyo.

Mfano Kama watu walikuwa na njaa mbaya sana kiasi cha kula kichwa cha punda au kiasi cha wanawake kula watoto wao kwa zamu, kisha ghafla watu hao wakatangaziwa kuwa mahindi, au ngano au unga au chakula kitapatikana kwa bei nafuu sana basi hiyo ni habari njema angalia mfano  ona

2Wafalme 6:24-30 “Ikawa baada ya hayo, Ben-hadadi mfalme wa Shamu akakusanya majeshi yake yote, akakwea akauhusuru Samaria. Njaa ikawa kuu huko Samaria; na tazama, wakauhusuru, hata kichwa cha punda kikapata kuuzwa kwa vipande themanini vya fedha, na kibaba cha mavi ya njiwa kwa vipande vitano vya fedha. Ikawa mfalme wa Israeli alipokuwa akipita ukutani, mwanamke mmoja akamwita akisema, Unisaidie, bwana wangu, mfalme. Akasema, Bwana asipokusaidia, nikusaidieje mimi? Ya sakafuni, au ya shinikizoni? Mfalme akamwambia, Una nini? Akajibu, Mwanamke huyu aliniambia, Mtoe mtoto wako, tumle leo, na mtoto wangu tutamla kesho. Basi, tukamtokosa mtoto wangu, tukamla; nikamwambia siku ya pili, Mtoe mtoto wako, tumle; naye amemficha mtoto wake. Ikawa, mfalme alipoyasikia maneno ya huyo mwanamke, aliyararua mavazi yake; (naye alikuwa akipita juu ya ukuta;) na watu wakaona, na tazama, alikuwa amevaa magunia ndani mwilini mwake.”

2Wafalme 7:1-11 “Elisha akasema, Lisikieni neno la Bwana; Bwana asema hivi, Kesho panapo saa hii, kipimo cha unga mzuri kitauzwa kwa shekeli, na vipimo viwili vya shayiri kwa shekeli, langoni pa Samaria. Basi yule akida, ambaye mfalme alikuwa akitegemea mkono wake, akamjibu yule mtu wa Mungu, akasema, Tazama, kama Bwana angefanya madirisha mbinguni, je! Jambo hili lingewezekana? Akamwambia, Angalia, wewe utaliona kwa macho yako, lakini hutakula. Basi walikuwapo watu wanne wenye ukoma, penye lango la mji; wakasemezana, Mbona tunakaa hapa hata tufe? Tukisema, Tutaingia mjini, mjini mna njaa, nasi tutakufa humo; nasi tukikaa hapa, tutakufa vile vile. Haya! Twende tukaliendee jeshi la Washami; wakituhifadhi hai tutaishi; wakituua, tutakufa tu. Basi wakaondoka kabla ya mapambazuko, ili waende mpaka kituo cha Washami; na walipofika mwanzo wa kimo cha Washami, kumbe! Hapana mtu. Kwa maana Bwana alikuwa amewasikizisha Washami kishindo cha miendo ya magari, na kishindo cha farasi, kama kishindo cha jeshi kubwa; wakaambiana, Tazama, mfalme wa Israeli amewaajiri wafalme wa Wahiti, na wafalme wa Wamisri, waje wapigane nasi. Kwa hiyo wakaondoka, wakakimbia kungali giza bado, wakaziacha hema zao, na farasi zao, na punda zao, na kimo chao vile vile kama kilivyokuwa, wakakimbia wapate kujiponya nafsi zao. Basi wale wenye ukoma walipofika mwisho wa kituo, waliingia katika hema moja, wakala, na kunywa, wakachukua fedha, na dhahabu, na mavazi, wakaenda wakavificha; wakarudi, wakaingia katika hema ya pili, vile vile wakachukua vitu, wakaenda, wakavificha. Ndipo wakaambiana, Mambo haya tufanyayo si mema; leo ni siku ya HABARI NJEMA, na sisi tunanyamaza; mkingoja hata kutakapopambazuka, madhara yatatupata; basi twende tukawaambie watu wa nyumba ya mfalme. Basi wakaenda, wakawaita mabawabu wa mji; wakawaambia, Tulifika kituo cha Washami, na tazama, hapana mtu ye yote huko, wala sauti ya mtu, ila farasi wamefungwa, na punda wamefungwa, na hema zao kama walivyoziacha. Na mabawabu wakaita wakawaambia watu wa nyumba ya mfalme.”

Unaweza kuona ukilinganisha hapo juu habari mbaya ya njaa mbaya iliyokuwepo zamani za Nabii Elisha na tangazo la Nabii Elisha na muujiza wa wale wakoma waliovumbua kuweko kwa chakula uvumbuzi kuhusu kuweko kwa chakula katika Samaria wakati kukiwa na njaa mbaya iliyopelekea wanawake kula watoto ilikuwa ni habari njema!

Ulimwengu tulio nao umeharibika, shetani na malaika zake wameiharibu dunia, uadilifu wa mwanadamu umeathiriwa, uhusiano wa Mungu na mwanadamu umeharibika, wanadamu wote tunafahamu kuwa tumeharibikiwa hatustahili tena kuwa na uhusiano na Mungu, tunastahili hukumu ya Mungu, tunastahiki kifo tunastahili adhabu, tunastahili kutupwa motoni, tunastahili kuharibiwa, tunastahili kukataliwa hatufai kwa sababu hakuna mtu mwenye nia ya kutafuta uhusiano mwema na Mungu tumeharibika tumeoza wanadamu wote kama yasemavyo maandiko ona

Warumi 3:10-12 “kama ilivyoandikwa, ya kwamba, Hakuna mwenye haki hata mmoja. Hakuna afahamuye; Hakuna amtafutaye Mungu. Wote wamepotoka, wameoza wote pia; Hakuna mtenda mema, la! Hata mmoja.”

Katika mazingira kama haya ya haribiko kubwa la mwanadamu anapotokea Mtu anatangaza kuwa Mungu amesamehe maovu yetu yote kwa sharti  moja tu na  sharti hilo ni kumuamini Mwanaye ambaye yeye alimtoa aadhibiwe yeye kwa niaba yetu pale msalabani na kuwa kazi tunayotakiwa sisi ni kuamini tu, na kuamini ni kukubali tu na kukiri na kushukuru na kwa kuamini huko hatutahukumiwa na tunahesabika kuwa watoto wa Mungu tukipewa haki sawa na mtoto wake aliyeishi maisha ya haki hizo sasa zinakuwa ni habari njema kwetu! unaona

Yohana 3:16-18 “Kwa maana jinsi hii Mungu aliupenda ulimwengu, hata akamtoa Mwanawe pekee, ili kila mtu amwaminiye asipotee, bali awe na uzima wa milele.  Maana Mungu hakumtuma Mwana ulimwenguni ili auhukumu ulimwengu, bali ulimwengu uokolewe katika yeye. Amwaminiye yeye hahukumiwi; asiyeamini amekwisha kuhukumiwa; kwa sababu hakuliamini jina la Mwana pekee wa Mungu.”

Unaona sasa kupitia kazi hii aliyoifanya baba kwa upendo wake tukimuamini mwana wake tumeokolewa, tunasamehewa hatuhukumiwi hizi ni habari njema ambazo kila mwanadamu zinapaswa kumfikia na ni kwa sababu ya haya Kristo alikuja ulimwenguni na kutoka katika kuamini tunasimama imara na kuokolewa, na kusamehewa na kubadilishwa mwenendo wa tabia na maisha yetu kwa neema tu kupitia nini kupitia kazi aliyoifanya Yesu pale msalabani

1Wakorintho 15:1-4 “Basi, ndugu zangu, nawaarifu ile injili niliyowahubiri; ambayo ndiyo mliyoipokea, na katika hiyo mnasimama, na kwa hiyo mnaokolewa; ikiwa mnayashika sana maneno niliyowahubiri isipokuwa mliamini bure. Kwa maana naliwatolea ninyi hapo mwanzo yale niliyoyapokea mimi mwenyewe, ya kuwa Kristo alikufa kwa ajili ya dhambi zetu, kama yanenavyo maandiko; na ya kuwa alizikwa; na ya kuwa alifufuka siku ya tatu, kama yanenavyo maandiko;”

Umuhimu wa kufanya uinjilisti.

Kusudi kubwa la Mungu kumtoa mwana wake wa pekee kuja ulimwenguni ni ili apate kuwaokoa wanadamu watakaomwamini, na wale wote ambao hawataamini watahukumiwa

Yoahana 3:16-18 “Kwa maana jinsi hii Mungu aliupenda ulimwengu, hata akamtoa Mwanawe pekee, ili kila mtu amwaminiye asipotee, bali awe na uzima wa milele. Maana Mungu hakumtuma Mwana ulimwenguni ili auhukumu ulimwengu, bali ulimwengu uokolewe katika yeye.  Amwaminiye yeye hahukumiwi; asiyeamini amekwisha kuhukumiwa; kwa sababu hakuliamini jina la Mwana pekee wa Mungu.”

Sasa ili watu waweze kukolewa ilikuwa ni lazima waisikie injili na wakiisha kuisikia injili, waiamini na wakiamini kwa maneno na vitendo yaani kubatizwa na kuwa wanafunzi wa Yesu na kusimama katika imani waokolewe, kwa hiyo tunajifunza ya kwamba watu hawawezi kuamini mpaka wasikie tena wasikie habari za Yesu

Marko 16:15-16 “Akawaambia, Enendeni ulimwenguni mwote, mkaihubiri Injili kwa kila kiumbe.  Aaminiye na kubatizwa ataokoka; asiyeamini, atahukumiwa.”

Habari za Yesu Kristo ni lazima zihubiriwe kwa jamii ya watu wote ulimwenguni, kama watu wanamtii Yesu kristo hili ni agizo la muhimu mno, na Mungu anataka tuliangalie kwa jicho la kipekee Yesu mwenyewe hapa anasema aaminiye ataokoka asiyeamini Atahukumiwa ni Dhahiri kuwa hukumu ipo na kama hatutaki watu waangukie katika hukumu ya Mungu basi hatuna budi kuihubiri injili na kuhakikisha watu wote duniani na kila jamii na taifa na kabila na lugha wanafikiwa na injili, wajibu huu wa kuihubiri injili ni wa watu wote na sio watumishi pake yao, Nyakati za kanisa la kwanza walihubiri kila mahali, na walitimiza wajibu wao sisi nasi hatuna budi kufanya hivyo ona

Matendo 8: 4-5 “Lakini wale waliotawanyika wakaenda huko na huko wakilihubiri neno. Filipo akatelemka akaingia mji wa Samaria, akawahubiri Kristo.”

Ikiwa watu wa Karne ya kwanza waliweza kuihubiri injili kwa miguu yao, kwa majahazi, kwa punda na farasi, wakati wa leo tunaweza kuwafikiwa watu kwa njia nyingi na za rahisi zaidi, tunaweza kuifanya kazi hii kwa wepesi na kuwafikiwa watu wengi sana Duniani, shime kila mahali nawaomba wakristo tuamke na kuieneza habari njema ya Bwana wetu Yesu Kristo kwani mavuno yako tayari na ni sisi tu ambao tunaweza kuueneza moto wa injili kwa njia zozote zile ambazo Mungu ametupa katika karne hii, Tunaweza pia kutoa fedha zetu, kununua vyombo vya injili, vyombo vya usafiri, vyombo vya kuhubiria ndani na vile vya kuhubiria nje, kujenga makanisa, kununua mahema, kufadhili vipindi vya redio nan television zinazohubiri injili pamoja na fadhila nyingine za aina nyingi sana za kuhakikisha kuwa tunamtaja na kumueneza Yesu kwa kila mwanadamu, Baraka kubwa sana italifunika kanisa na taifa na jamii yoyote ile itakayotumia kila njia kuhakikisha kuwa injili inawafikia watu wote, hili ni agizo la Bwana wetu Yesu kwa kanisa lake kila mahali duniani, watu wa Mungu wako tayari na wana kiu lakini wanalisubiria kanisa liamke na kuupeleka moto wa injili haleluyaaa

Warumi 10:14-17 “Basi wamwiteje yeye wasiyemwamini? Tena wamwaminije yeye wasiyemsikia? Tena wamsikieje pasipo mhubiri? Tena wahubirije, wasipopelekwa? Kama ilivyoandikwa, Ni mizuri kama nini miguu yao wahubirio habari ya mema! Lakini si wote walioitii ile habari njema. Kwa maana Isaya asema, Bwana, ni nani aliyeziamini habari zetu? Basi imani, chanzo chake ni kusikia; na kusikia huja kwa neno la Kristo.”

Kuhubiri injili ni sawa na kuunga umeme katika miji yote isiyo na umeme, ni kuwasha nuru maeneo yote yenye giza, kama hatutaihubiri injili watu wataamini mambo ya giza, watafuata falsafa nyingine, watatambikia mizimu, wataabudu dini za uongo, watafuata mafundisho ya imani nyingine mbaya na zisizo na ustaarabu, wote tumekuwa mashahidi kuwa kila mahali injili ilipoingia kumekuwa na maendeleo makubwa ya kitaaluma, kiuchumi na kiuadilifu na ustaarabu na maeneo mengi ambayo injili haijafika kumekuwapo giza Kuu, kokote Yesu anakopelekwa ni dhahiri kuwa nuru kubwa iliwazukia watu wa jamii hiyo;-

Mathayo 4:13-16 “akatoka Nazareti, akaja akakaa Kapernaumu, mji ulioko pwani, mipakani mwa Zabuloni na Naftali; ili litimie neno lililonenwa na nabii Isaya, akisema, Nchi ya Zabuloni na nchi ya Naftali, Njia ya bahari, ng'ambo ya Yordani, Galilaya ya mataifa, Watu wale waliokaa katika giza Wameona mwanga mkuu, Nao waliokaa katika nchi na uvuli wa mauti Mwanga umewazukia.”

Kwa msingi huo mpendwa hatuna budi kuipeleka nuru ya Yesu, kwa kuhakikisha kuwa tunawaeleza watu wote habari njema, acha kuhisi kuwa aaa siku hizi watu wanasikia bhana, hapana fanya wajibu wako wa kuihubiri injili na kama mtu yuko kimya muhubirie injili mpaka aseme mimi ni muamini mwenzako, eee kama umekaa kimya tutajuaje kuwa umeokoka tayari? Lihubiri neno.  Kumbuka kuwa katika wakati tulio nao ni rahisi zaidi kuhubiri injili

Tuige mifano ya watu mbalimbali ambao waliihubiri injili, Billy Graham anasemekana kuwa ndiye mwanadamu aliyeihubiri injili kwa watu wengi sana kiasi cha kuitwa muhubiri mkubwa wa karne ya 20, alihubiri mikutano mbalimbali ya ndani na nje huku mahubiri yake yakirushwa katika redio na television mbalimbali duniani  na matokeo yake Grahamu amekuwa Muhubri ambaye amehubiria watu wengi zaidi kuliko wote katika historia ya Ukristo na kwa rekodi za maafisa wake watu wapatao milioni 3.2 waliwahi kumpiokea Yesu katika mahubiri yake alihubiri injili katika maisha yeke tangu mwaka 1947 – 2005 alipostaafu. Amehubiria zaidi ya watu milioni 215 na amehubiri katika inchi zaidi ya 185, kwa mikutano zaidi ya 400 yeye anatupa changamoto leo kufanya kila tuwezalo kulifanya kuhakikisha kuwa dunia inajawa na injili, hakuwa na mbwembwe, alihubiri kwenye madhabahu akiwa na uso mkali na sauti yenye mamlaka akiwa na ushawishi mkubwa wa kuwafanya watu watubu na maelfu ya watu walikuwa wakitubu katika kila mkutano wake, alifariki Tarehe 21 February 2018 akiwa na umri wa miaka 99  

Madhara ya kuacha kuhubiri injili.

Kutokuihubiri injili ni UASI ni DHAMBI ni kwenda kinyume na maagizo ya Mungu!  Kwa sababu kwa namna moja ama nyingine tutakuwa tu mechangia uharibifu kwa dunia ambayo kama ingesikia habari njema Yesu angewaokoa, Nyakati za agano la kale Mungu alipowatuma manabii kufanya kazi ya kuonya na manabii hao walionywa pia kuwa wasiposema Mungu atawahukumu wao kwa sababu wameacha kuwa wasemaji kwa niaba ya Mungu,

Ezekiel 3:18 -19. “Nimwambiapo mtu mbaya, Hakika utakufa; wewe usimpe maonyo, wala husemi na huyo mtu mbaya ili kumwonya, kusudi aache njia yake mbaya na kujiokoa roho yake; mtu yule mbaya atakufa katika uovu wake; lakini damu yake nitaitaka mkononi mwako. Lakini ukimwonya mtu mbaya, wala yeye hauachi ubaya wake, wala njia yake mbaya, atakufa katika uovu wake; bali wewe umejiokoa roho yako.”   

Ezekiel 33:7-9 “Basi wewe, mwanadamu, nimekuweka kuwa mlinzi kwa nyumba ya Israeli; basi ulisikie neno hili kinywani mwangu, ukawape maonyo yangu.  Nimwambiapo mtu mbaya, Ewe mtu mbaya, hakika utakufa, nawe husemi neno la kumwonya mtu huyo, aiache njia yake, mtu mbaya huyo atakufa katika uovu wake, lakini damu yake nitaitaka mkononi mwako. Walakini ukimwonya mtu mbaya kwa sababu ya njia yake, kusudi aiache; wala yeye asiiache; atakufa huyo katika uovu wake, lakini wewe umejiokoa roho yako.”             

Neno la Mungu bado linatuonya ya kuwa tunawajibu wa kuwaeleza watu habari njema, mtazamo unaweza kuwa tofauti na wakati wa Agano la kale ambapo manabii walipeleka maonyo tu na kusisitiza toba, lakini ujumbe wetu sisi ni mwepesi sana ukilinganisha na nyakati za agano la kale sisi tunapaswa kuwaeleza watu habari njema na sio za vitisho, kuwaeleza watu habari za upendo wa Yesu, habari za msamaha wa dhambi bure na kwa neema tu, Habari ya kuwa Yesu alisulubiwa akafa akazikwa kwa niaba yetu nao wataokolewa, lakini kwa kuwa Mungu habadiliki kama hatutaihubiri injili tunakuwa tumewafungia watu malango ya ufalme na tutawajibika na kuhukumiwa kwa kutokumtii Mungu kwa kufikisha agizo lake, ni nyepesi sana kwa sababu sio sisi tunaookoa anaeokoa ni yeye mwenyewe lakini sisi ni wajumbe wake, Kila kanisa kila mkristo aliye hai ana wajibu wa kuihubiri injili na tusipofanya hivyo tutawajibishwa na kuhukumiwa kama ilivyokuwa maonyo ya Mungu kwa Ezekiel na Paulo mtume

1Wakorintho 9:16-17 “Maana, ijapokuwa naihubiri Injili, sina la kujisifia; maana nimewekewa sharti; tena ole wangu nisipoihubiri Injili! Maana nikiitenda kazi hii kwa hiari yangu nina thawabu; ila ikiwa si kwa hiari yangu, nimeaminiwa uwakili.”

Ndani ya habari njema kuna uweza na nguvu za Mungu zenye kuokoa kwa hiyo wajibu wetu ni kuipeleka ni kusema ni kutangaza, muhubiri Yesu waeleze watu habari za Yesu na uweza wa kuokoa ni wake naye atafanya !.

Warumi 1:16- “Kwa maana siionei haya Injili; kwa sababu ni uweza wa Mungu uuletao wokovu, kwa kila aaminiye, kwa Myahudi kwanza, na kwa Myunani pia.”

Namna nyepesi ya kuifikisha injili

Muhubiri Kristo!, hubiri kazi yake ya huruma aliyoifanya pale msalabani, nyakati za kanisa la kwanza hawakuwa na maneno mengi zaidi ya kuthibitisha kuwa Yesu aliteswa kwaajili yetu alikufa na siku ya tatu akafufuka, huyu ni Mwana wa Mungu, huyu anaokoa, huyu anasamehe dhambi, bila kujali kuwa dhambi zetu zilikuwa nyekundu kama damu, yeye alijiadhibu mwenyewe msalabani kwaajili yetu.

Matendo 8: 4-5 “Lakini wale waliotawanyika wakaenda huko na huko wakilihubiri neno. Filipo akatelemka akaingia mji wa Samaria, akawahubiri Kristo.”

Zingatia misingi minne tu wakati unapoisema habari njema kwa njia rahisi ya kumuelezea mtu mmoja mmoja habari za kristo

1.       Wote tumefanya dhambi na kupungukiwa na utukufu wa Mungu Warumi 3:23-24 “kwa sababu wote wamefanya dhambi, na kupungukiwa na utukufu wa Mungu; wanahesabiwa haki bure kwa neema yake, kwa njia ya ukombozi ulio katika Kristo Yesu;”

2.       Afichaye dhambi zake hatafanikiwa aziungamaye na kuziacha atapata Rehema Mithali 23:13-14 “Afichaye dhambi zake hatafanikiwa; Bali yeye aziungamaye na kuziacha atapata rehema. Mwanadamu mwenye kicho yu heri sikuzote; Bali mshupavu wa moyo ataangukia madhara.”            

3.       Tukiziungama dhambi zetu yeye ni mwaminifu atatusamehe 1Yohana 1;9Tukiziungama dhambi zetu, Yeye ni mwaminifu na wa haki hata atuondolee dhambi zetu, na kutusafisha na udhalimu wote.”         

4.       Mwamini Bwana Yesu na utaokoka wewe pamoja na nyumba yako  yaani Familia yako na jamaa zako Matendo 16: 30-32. “kisha akawaleta nje akasema, Bwana zangu, yanipasa nifanye nini nipate kuokoka? Wakamwambia, Mwamini Bwana Yesu, nawe utaokoka pamoja na nyumba yako. Wakamwambia neno la Bwana, yeye na watu wote waliomo nyumbani mwake.”

Ikiwa mtu atakubali kujitambua kuwa sisi wote ni wakosaji, na kuwa tunahitaji rehema za Mungu, na kuwa rehema hizo zinapatikana kwa kazi aliyoifanya Yesu pale msalabani na kuwa wajibu wetu ni kuamini tu, mtu huyo akikubali kuamini atasema maneno haya

Bwana Yesu ninakushukuru kwa kuwa nimesikia neno lako, na nimeamini kazi uliyoifanya pale msalabani, nakushukuru kwa kuwa wewe ni bwana na kwa upendo wa Mungu umeniokoa na kunisamehe mimi nisiyestahili, nakuamini wewe kwa msamaha wa uovu wangu wote Amen

Kwa sala hii mtu huyo atakuwa amemuamini Bwana na atapaswa kuwa mwanafunzi wa Yesu kwaajili ya mafundisho na maelekezo mengine zaidi, Amen

Rev. Innocent Kamote

Mkuu wa wajenzi mwenye Hekima!.

Ijumaa, 17 Novemba 2023

Baba yangu na mama yangu wameniacha


Zaburi 27:9-11 “Usinifiche uso wako, Usijiepushe na mtumishi wako kwa hasira. Umekuwa msaada wangu, usinitupe, Wala usiniache, Ee Mungu wa wokovu wangu. Baba yangu na mama yangu wameniacha, Bali Bwana atanikaribisha kwake. Ee Bwana, unifundishe njia yako, Na kuniongoza katika njia iliyonyoka; Kwa sababu yao wanaoniotea;”




Utangulizi:

Watu wote tunaweza kuwa na ufahamu wa kutosha kuhusiana na swala zima la Umuhimu wa Baba na Mama yaani wazazi wetu na walezi wetu, kwa jinsi walivyo wa Muhimu sana Duniani, Wazazi wetu na walezi wetu wana mchango mkubwa sana na wa muhimu sana katika kutuleta Duniani na uangalifu wao mkubwa wa kuhakikisha tunapata malezi na kukua tukiwa na furaha na Amani, wao pia hujitahidi sana katika kuhakikisha wanatutimizia mahitaji yetu, wanatunza afya zetu wanaonyesha kujali na nafikiri hata kabla ya kumjua Mungu kwa kawaida tunaanza kuwajua wao, wao ni wa Muhimu sana kama hujui umuhimu wa wazazi baba na mama na walezi Hebu wapoteze siku moja ndipo utakapoingia katika wimbi la kujua uchungu wa dunia, mimi nilipoteza mama yangu nikiwa mdogo sana mpaka leo moyo wangu umejawa na majonzi makubwa mno siwezi kumkufuru Mungu kwa kutokuwepo kwake lakini wakati mwingine hata katika utu uzima huu huwa nasema laiti mama yangu angelikuwepo nadhani unaelewa! Nataka tu kuonyesha umuhimu wa watu hawa, na ndio maana Mungu katika Hekima yake anataka watu hawa wapewe heshima maalumu na ya tofauti katika maandiko na kuwa kupitia wao kunakuwa na Baraka kubwa sana katika maisha yetu ona

Waefeso 6:1-3 “Enyi watoto, watiini wazazi wenu katika Bwana, maana hii ndiyo haki. Waheshimu baba yako na mama yako; amri hii ndiyo amri ya kwanza yenye ahadi,Upate heri, ukae siku nyingi katika dunia.”

Unaona tuwapo Duniani wazazi ni nguzo ya ulinzi na usalama wa maisha yetu duniani, kama utakuwa umeishi katika nyumba ambayo baba na mama wameachana au kuna mafarakano yaliyopelekea mmoja akaondoka au ukibaki yatima unaweza kujua umuhimu wa uwepo wa wazazi ndipo sa Maandiko yanatuasa tuwaheshimu sana kwani kwa kufanya hivyo tunapata Baraka na mafanikio na kupewa uwezo wa kuishi siku nyingi duniani, Hata hivyo katika mazingira Fulani wazazi wetu wanaweza kutuacha na tukajikuta tumebaki wenyewe na ni mmoja tu anayeweza kubaki na uaminifu wake mpaka dakika ya mwisho yaani Mungu wetu wa Mbinguni, hilo ndilo ambalo Mwandishi wa zaburi anataka kutuonyesha leo:-

·         Maana  ya neno kuachwa

·         Baba yangu na mama yangu wameniacha!

·         Bali Bwana atanikaribisha kwake !

Maana ya neno Kuachwa!

Zaburi 27:9-11 “Usinifiche uso wako, Usijiepushe na mtumishi wako kwa hasira. Umekuwa msaada wangu, usinitupe, Wala usiniache, Ee Mungu wa wokovu wangu. Baba yangu na mama yangu wameniacha, Bali Bwana atanikaribisha kwake. Ee Bwana, unifundishe njia yako, Na kuniongoza katika njia iliyonyoka; Kwa sababu yao wanaoniotea;”

Ni Muhimu kufahamu kuwa neno kuachwa linalotumika hapo katika maandiko ya Kiebrania linasomeka kama  AZAB ambalo kwa kiingereza wanatumia neno FORSAKEN  Lakini kimsingi neno linalopaswa kutumika hapo ili kuleta maana inayokusudiwa ni neno ABANDONED ambalo ufafanuzi wake ni cease to support or look after someone kwa Kiswahili ni KUTELEKEZA wakati neno Forsaken ni kuacha, kwa hiyo kimsingi neno ambalo Daudi analimaanisha hapo ni KUTELEKEZWA  kwa hiyo kuachwa ni jambo lingine na kutelekezwa ni swala lingine na ni zaidi ya kuachwa!, Kama mtu aliyekuwa amejenga nyumba ya thamani sana kisha akaacha kuihudumia na kuiacha ikawa ka ma gofu au mahame!

Neno kutelekeza linatumika katika Kiswahili kumaanisha Mtu anayetegemewa kutoa msaada wa matumizi, malezi, chakula mavazi na matibabu, makazi ulinzi pamoja na mahitaji yote ya msingi anapopotea au kuacha kutoa huduma hizo au kuacha kujihusisha na wale wanaomtegemea na kuwaacha wakiwa hawana msaada. Wzazi wetu wa kiroho pia wanaweza kufanya hivyo yaani kututelekeza!

Baba yangu na mama yangu wameniacha!

Zaburi 27:9-11 “Usinifiche uso wako, Usijiepushe na mtumishi wako kwa hasira. Umekuwa msaada wangu, usinitupe, Wala usiniache, Ee Mungu wa wokovu wangu. Baba yangu na mama yangu wameniacha, Bali Bwana atanikaribisha kwake. Ee Bwana, unifundishe njia yako, Na kuniongoza katika njia iliyonyoka; Kwa sababu yao wanaoniotea;”

Kimsingi hatuna uhakika kama kuna mahali ambapo Daudi aliwahi kutelekezwa na baba yake na mama yake, Japo tunaweza tu kukumbuka tukio la Daudi kuachwa akiwachunga kondoo wa babaye wakati Samuel alipokuja kutawadha mtu atakayekuwa mfalme kutoka katika familia ya Yese ona

1Samuel 16:11-13 “Kisha Samweli akamwambia Yese, Watoto wako wote wapo hapa? Naye akasema, Amesalia mdogo wao, na tazama, anawachunga kondoo. Basi Samweli akamwambia Yese, Tuma watu, wamlete; kwa sababu hatutaketi hata atakapokuja huku. Basi akatuma mtu, naye akamleta kwao. Naye alikuwa mwekundu, mwenye macho mazuri, na umbo lake lilikuwa la kupendeza. Bwana akasema, Ondoka, umtie mafuta; maana huyu ndiye. Ndipo Samweli akaitwaa pembe yenye mafuta, akamtia mafuta kati ya ndugu zake; na roho ya Bwana ikamjilia Daudi kwa nguvu tangu siku ile. Basi Samweli akaondoka, akaenda zake Rama.”  

Hapa tunaweza tu kupata mwanga kwamba Daudi alipuuziwa ukilinganisha na ndugu zake wengine japo ukweli ni kuwa Mungu alikuja kumchagua yeye, hatuwezi kusema kuwa Daudi alitelekezwa, aidha wakati wa taabu zake alikimbia pamoja na wazazi wake na baadaye aliona ni vema akawahifadhi kwa Mfalme wa Moabu yaani kwa ndugu wa bibi yake RUTHU ambako aliwahifadhi wazazi wake kwa muda ili wasikutane na misukosuko ya kukimbia huku na huko

 1Samuel 22:3-4 “Kutoka huko Daudi akaenda Mispa ya Moabu; akamwambia mfalme wa Moabu, Tafadhali ukubali baba yangu na mama yangu watoke huko waliko, wakakae kwenu, hata nitakapojua Mungu atakalotenda kwa ajili yangu. Akawaleta mbele ya mfalme wa Moabu, nao wakakaa pamoja naye wakati wote Daudi alipokuwa ngomeni.”

Hapa pia hatuoni ushahidi wa Daudi kuachwa au kutelekezwa na Familia yake kwanini Daudi anazungumza katika zaburi hii kuwa baba yangu na mama yangu wameniacha Lakini Bwana atanikaribisha kwake ? hii ilikuwa ni lugha ya kimashairi ambayo Daudi aliitumia kutufundisha jambo kuhusu utendaji wa Mungu, Daudi anataka kuonyesha wasikilizaji wake kuwa hata pamoja na ukaribu mkubwa walio nao wazazi wetu na walezi wetu na uwezo wao na uchungu wao mkubwa wa kutuhudumia, bado Mungu anabaki kuwa msaada ulio karibu zaidi kuliko msaada wa wazazi, anataka kuonyesha kuwa utendaji wa Mungu katika maisha yetu unazidi ule  wa wazazi, kwani  wao pamoja na kujitoa kwao na kujidhabihu kwao kuna wakati wanaweza kuacha kuwa na huruma dhidi yetu lakini sivyo alivyo Bwana Mungu wetu, wale wote wanaodhani ya kuwa Mungu amewatelekeza wanapaswa kujua kuwa wazazi baba na mama wanaweza kufanya tukio hilo lakini sio ilivyo kwa Bwana Mungu wetu ona

Isaya 49:14-16. “Bali Sayuni alisema, YEHOVA ameniacha, Bwana amenisahau.  Je! Mwanamke aweza kumsahau mtoto wake anyonyaye, hata asimhurumie mwana wa tumbo lake? Naam, hawa waweza kusahau, lakini mimi sitakusahau wewe. Tazama, nimekuchora katika vitanga vya mikono yangu; kuta zako ziko mbele zangu daima.”

Na ndio maana inapotokea Mtu amepoteza mume, au amepoteza wazazi na kuwa yatima Mungu mwenyewe huchukua nafasi hiyo na kuwa mume wa wajane na baba wa yatima ona

Zaburi 68:5-6 “Baba wa yatima na mwamuzi wa wajane, Mungu katika kao lake takatifu. Mungu huwakalisha wapweke nyumbani; Huwatoa wafungwa wakae hali ya kufanikiwa; Bali wakaidi hukaa katika nchi kavu.”

Wakati wote katika maisha yetu, tunapohisi kutelekezwa, au kuachwa au kuwa peke yetu hakuna sababu ya kuumia na kuteseka tukijuliza kuwa Msaada (wokovu) wetu utatokea wapi Mungu aliye baba wa wapweke baba wa Yatima mwamuzi wa wajane atatuletea wokovu mkuu

Hosea 14:3 “Ashuru hatatuokoa; hatutapanda farasi; wala hatutaiambia tena kazi ya mikono yetu, Ninyi ndinyi miungu yetu; maana kwako wewe wasio na baba hupata rehema.”

Mungu atachukua jukumu la baba na mama au walezi kwa kila anayemuamini, ataonyesha upendo wake usiokoma  na ataonyesha kujali  katika namna ambayo mwanadamu hawezi kuifanya, kimsingi katika lugha hii kwa sababu ni ya kimashairi Daudi katika lugha ya kawaida anazungumza kuwa HATA KAMA  baba yangu na mama yangu wataniacha Mungu atachukua nafasi  na ni mwenye nafasi ya kuonyesha anajali zaidi ya ukaribu walio nao wazazi wetu  yeye hatakuja kutuacha wala kutupungukia na tunaweza kuliitia jina lake katika mazingira magumu kama hayo!, na sio baba na mama peke yao awaye yote tunayemtegemea katika maisha haya akitutelekeza Mungu aliyetuumba na aliye baba mwema anachukua jukumu kubwa la kutuweka mabegani mwake katika ulimwengu wa roho na kuonyesha kujali kuliko karibu zaidi ya mwanadamu wa kawaida

Bali Bwana atanikaribisha kwake !

Kwa kawaida Bwana hukaribisha kwake watu wa aina yoyote ile  hata wale ambao wamekataliwa kwa sababu zozote zile katika jamii, hakuna mtu mwema na mzuri sana kiasi cha kumshawishi Mungu kumkubali wala hakuna mtu mbaya sana kiasi cha kumshawishi Mungu kumkataa, yeye alisema katika neno lake kuwa yeyote ajaye kwake hatamtupa nje kamwe

Yohana 6:37 “Wote anipao Baba watakuja kwangu; wala ye yote ajaye kwangu sitamtupa nje kamwe.”

Kristo Yesu alipokuwa duniani aliwakaribisha watu wengi sana kwake hata wale waliokuwa wamekataliwa na jamii

Luka 15:1-2 “Basi watoza ushuru wote na wenye dhambi walikuwa wakimkaribia wamsikilize. Mafarisayo na waandishi wakanung'unika, wakisema, Mtu huyu huwakaribisha wenye dhambi, tena hula nao.”

Neno kukaribisha katika biblia ya kiyunani linasomeka kama neno PROSLAMBANO/PROSDECHOMAI  na kwa Kiebrania ni ASAPH  ambalo maana zake ni Kuhudumia, kukubali, kuwaangalia, kuwapokea, kuwatambua, kuwakusanya,  Wakati wote milango ya Mungu iko wazi kutukaribisha kwake na tukawa kwake watoto wake na wanae, Kuachwa kwa aina yoyote ile kutakakokupata Duniani kusikufanye wewe ukajisikia kuwa una bahati mbaya, kutelekezwa kwako kwa aina yoyote ile kusikufanye wewe ukajisikia kuwa huna thamani yuko Mungu mbinguni ambaye ndiye aliyekuumba yeye anakuthamini kuliko unavyoweza kufikiri alishatuahidi ya kuwa hatatuacha wala hatatupungukia

Yoshua 1:5 “Hapatakuwa mtu ye yote atakayeweza kusimama mbele yako siku zote za maisha yako; kama nilivyokuwa pamoja na Musa, ndivyo nitakavyokuwa pamoja na wewe; sitakupungukia wala sitakuacha.”

Zamani sana tulikuwa tunaimba Baba na mama wawezakuniacha, lakini Yesu hawezi kuniacha, Rafiki zangu waweza kuniacha lakini Yesu hawezi kuniacha!

 

Rev. Innocent Kamote.

Mkuu wa wajenzi mwenye Hekima


Jumanne, 14 Novemba 2023

Wafariji wenye kutaabisha.


Ayubu 16:1-6 “Ndipo Ayubu akajibu, na kusema, Nimesikia maneno mengi mfano wa hayo; Ninyi nyote ni wafariji wenye kutaabisha. Je! Maneno yasiyo faida yatakuwa na mwisho? Au, kuna nini kinachokukasirisha, hata ukajibu? Mimi nami ningeweza kunena kama ninyi; Kama roho zenu zingekuwa mahali pa roho yangu, Ningeweza kutunga maneno juu yenu, Na kuwatikisia ninyi kichwa changu. Lakini ningewatia nguvu kwa kinywa changu, Na utuzo wa midomo yangu ungetuliza. Nijapokuwa nanena, huzuni yangu haitulizwi; Nijapokuwa najizuia, nimepunguziwa kitu gani?


Utangulizi:

Kitabu cha Ayubu ni moja ya kitabu kilichoandikwa kwaajili ya kutoa majibu kwa ulimwengu kuhusu falsafa ya mateso, kwanini maisha ya mwanadamu hukutana na changamoto za aina mbalimbali, lakini sio hivyo tu kujibu pia swali kwanini wenye haki nao wanateseka?  Ayubu alikuwa mtu mwenye haki mbele za Mungu, hata hivyo alikumbana na mateso makubwa ya aina mbalimbali, ambayo aliyavumilia na mwisho wake ukawa mwema, Ayubu leo amekuwa mfano mzuri na mwema wa kuigwa katika swala zima la kuvumilia mateso na kuonyesha wema wa Mungu kwetu pale tunapovumilia, Mungu ni mwingi wa rehema na mwenye huruma

Yakobo 5:10-11 “Ndugu, watwaeni manabii walionena kwa jina la Bwana, wawe mfano wa kustahimili mabaya, na wa uvumilivu. Angalieni, twawaita heri wao waliosubiri. Mmesikia habari ya subira yake Ayubu, mmeuona mwisho wa Bwana ya kwamba Bwana ni mwingi wa rehema, mwenye huruma.”

Pamoja na mapito aliyokuwa akiyapitia Ayubu lakini vilevile Maandiko yanatufundisha kuwa wakati tunapopitia mambo magumu kwa kawaida wanakuwepo watu wanaokuja katika maisha yetu na kutoa ushauri/kufariji au kusema hili au lile kutokana na mapito tunayoyapitia wakati mwingine watu hao wakiwa na nia njema na wakati mwingine wakiwa hawajui wanachoweza kusema kuhusiana na mapito yako kama kiko sahihi au la kama ni mapenzi ya Mungu au la,  na wakati mwingine sio rahisi kujua siri ya mapito anayoyapitia mtu isipokuwa Mungu mwenyewe, wakati Ayubu alipokuwa akipitia wakati Mgumu neno linatueleza kuwa alitembelewa na rafiki zake watatu ambao walikuja kwa kusudi la kumfariji kutokana na mapito aliyokuwa anayapitia ona:-

 Ayubu 2:11-13 “Basi ikawa hao rafikize Ayubu watatu walipopata habari ya mabaya hayo yote yaliyomfikilia, wakaja kila mtu kutoka mahali pake; nao ni Elifazi Mtemani, na Bildadi Mshuhi, na Sofari Mnaamathi; wakapatana pamoja ili waende kumlilia Ayubu na kumtuliza moyo. Basi walipovua macho yao, nao wakali mbali, wasimtambue, wakainua sauti zao na kulia; kila mmoja akararua joho yake, wakarusha mavumbi juu ya vichwa vyao kuelekea mbinguni. Kisha wakaketi nchi pamoja naye muda wa siku saba, mchana na usiku, wala hapana mmoja aliyenena naye neno lo lote; kwa maana waliona ya kuwa mashaka yake aliyo nayo ni makuu mno.”                         

Elifazi Mtemani, Bildadi Mshuhi na Sofari mnaamathi walikuwa na nia njema na nzuri kabisa ya kumfariji Ayubu na mioyo yao na matendo yao yanadhihirisha kuwa walikuwa wako sahihi katika kutafuta namna ya kumfariji ndugu yao kutokana na mambo magumu aliyoyapitia, hata hivyo katika namna ya kushangaza sana baada ya wao kutoa hoja mbalimbali Ayubu aliwaita watu hao au rafiki zake kuwa ni WAFARIJI WENYE KUTAABISHA   angalia hapa Ayubu 16:2 “Nimesikia maneno mengi mfano wa hayo; Ninyi nyote ni wafariji wenye kutaabisha.” sasa swali kubwa kwetu na macho yetu ni kuliangalia jambo hili kwa kina na mapana na marefu kuwa wafariji wenye kutaabisha ni watu wa namna gani ?  na ni vipi tunaweza kukabiliana nao wanapojitokeza katika maisha yetu, na kama sisi nasi tunataka kuwa wafariji na washauri wa wengine ni tahadhari gani tunapaswa kuzizingatia. Tutajifunza somo hili kwa kuzingatia vipengele vitatu vifuatavyo:-

·         Maana ya Wafariji wenye kutaabisha

·         Jinsi Mtu anavyoweza kuwa mfariji mwenye kutaabisha

·         Namna ya kujiepusha na wafariji wenye kutaabisha au kuwa wafariji wenye kutaabisha

Maana ya Wafariji wenye kutaabisha:

Ayubu 16:1-6 “Ndipo Ayubu akajibu, na kusema, Nimesikia maneno mengi mfano wa hayo; Ninyi nyote ni wafariji wenye kutaabisha. Je! Maneno yasiyo faida yatakuwa na mwisho? Au, kuna nini kinachokukasirisha, hata ukajibu? Mimi nami ningeweza kunena kama ninyi; Kama roho zenu zingekuwa mahali pa roho yangu, Ningeweza kutunga maneno juu yenu, Na kuwatikisia ninyi kichwa changu. Lakini ningewatia nguvu kwa kinywa changu, Na utuzo wa midomo yangu ungetuliza. Nijapokuwa nanena, huzuni yangu haitulizwi; Nijapokuwa najizuia, nimepunguziwa kitu gani?

Moja ya swali muhimu la kujiuliza hapa ni kwanini Ayubu anawaita watu hawa kama wafariji wenye kutaabisha japo tunaweza kuwa na ufahamu kuwa walikuwa na nia nzuri na walijitahidi kwa kadiri ya hekima waliyokuwa nayo, kumtia moyo lakini mwisho wa yote walikuwa ni wafariji wenye kutaabisha na Mungu aliwakemea kuwa hawakunena sawasawa na Mungu wala sawasawa na Mtumishi wake Ayubu na hivyo walitakiwa kutoa dhabihu kuomba radhi kwa uovu wao!

Neno wafariji wenye kutaabisha kimsingi katika biblia ya kiingereza Mstari wa pili ambao ni wa msingi katika somo letu unasomeka hivi

I have heard many such things MISERABLE COMFORTERS  are ye all  neno MISERABLE   kwa kiibrania ni “AMAL” ambalo maana yake ni wenye kulaumu, wenye kukutendea vibaya, wenye unyanyasaji, wenye kuchosha, wenye kuumiza, wenye kuhuzunisha, wenye maumivu, wenye kuogopesha, wenye uovu, wenye kuchosha, wenye kutia uvivu, wenye kukatisha tamaa, wenye kuvunja moyo, wenye uovu, wasiyo na kweli, wenye kupotosha.  Neno hilo AMAL limetumika mara 55 Katika Biblia na katika mistari tofauti 54  

Kwa msingi huo Ayubu alikuwa anamaanisha kuwa ameshawasikia watu wengi kama hawa na kuwa katika faraja na ushauri waliokuwa wakijaribu kuutoa walikuwa wametoka nje ya makusudi na mpango wa Mungu kwa sababu hiyo badala ya kumfariji, walikuwa wakizungumza tu na kwa kweli walikuwa wametoka pia nje ya kusudi na ukweli kuhusu mtazamo wa Mungu, kwa ujumla walikuwa nje ya kweli ya Mungu, tena wala walikuwa hawawakilishi mfumo na sifa za Mungu, kwa hiyo Ayubu alipowasikiliza aliona wazi kuwa wanamkosea Mungu mno, walikuwa wanahisi tu jambo Fulani kuhusu utendaji wa Mungu wakati wa majaribu ya mtu lakini haikuwa kweli ya Mungu wala kusudi la Mungu na pia walikuwa wakimshutumu Mtumishi wa Mungu Ayubu kwamba ana kesi ya kujibu katika mabaya aliyokuwa anayapitia n ahata watoto wake waliokufa vibaya walikuwa na makosa Fulani na kwa sababu hiyo ingawa walikuja kwa wakati kwa kusudi la kumfariji na kumshauri  Ayubu walijikuta wanapotosha, wanamuumiza zaidi, wanamvunja moyo, wananena uovu, wanasema yasiyo kweli, wanamchosha na wanamuumiza hali kama hii inaweza kuwepo kwa watu wengi wanaotuzunguka katika nyakati zetu hata siku za leo!

Ayubu alikuwa amepitia majaribu makubwa na mazito mno kiasi cha kupatwa na mashaka makubwa sana, rafiki zake waliojitokeza kumfariji badala ya kumpunguzia maumivu aliyokuwa akiyapitia wao waliongeza huzuni na maumivu mtazamo wao kuhusu majaribu ulikuwa ukimtaka Ayubu akiri na kutubu dhambi zake ili Mungu aondoe adhabu aliyoiweka juu yake

Ayubu 11:14-17. “Ikiwa una uovu mkononi mwako, uweke mbali nawe, Wala usikubali upuzi kukaa hemani mwako; Hakika ndipo utakapopata kuinua uso pasipo ila; Naam, utathibitika, wala hutakuwa na hofu; Kwa kuwa utasahau mashaka yako; Utayakumbuka kama maji yaliyokwisha pita; Na maisha yako yatakuwa meupe kuliko adhuhuri; Lijapokuwa ni giza, litakuwa kama alfajiri.”

Ayubu 22:4-7 “Je! Ni kwa wewe kumcha yeye anakukemea? Na kuingia hukumuni nawe? Je! Uovu wako si mkuu? Wala maovu yako hayana mwisho. Kwa kuwa umetwaa dhamana kwa nduguyo bure, Na kuwavua nguo zao walio uchi. Hukumpa maji ya kunywa huyo aliyechoka, Nawe umemnyima chakula huyo mwenye njaa.”

Sio jambo la kushangaza hata katika siku zetu leo, pale tunapopatwa na mapito magumu, majaribu magumu na mitihani ya aina mbalimbali, wafariji wengi na washauri hukimbilia katika hatima ya kusema kuwa ni kwa sababu tu mefanya dhambi, au kuna kosa kubwa sana ambalo mtu amelifanya  na sio hivyo tu hata katika nyakati zetu leo watu wengi sana hufikiri kuwa mtu akiwa na mafanikio ya mwilini basi yuko vizuri na Mungu na mtu akiwa na majanga basi kutakuwa kuna shida katika mahusiano yake na Mungu  fikira za namna hii sio tu zinawakosesha amani wanaopita katika mapito bali pia zinaharibu mtazamo wa utendaji wa Mungu na kupotosha ukweli kuhusu utendaji wa Mungu!, badala ya watu kushauri vema na kukujenga wanakubomoa na kuichoma nafsi yako kiasi ambacho wanataka kukugombanisha wewe na Mungu, Wafariji wa namna hii huongezea Msiba wakati wa matatizo badala ya kukusaidia hao ndio wanaitwa wafariji wenye kutaabisha!

 

Jinsi Mtu anavyoweza kuwa mfariji mwenye kutaabisha

1.       Mtu anayefikiri kila mwanadamu anayeteseka ni kwa sababu amefanya dhambi -  Mfariji mwenye kutaabisha ni mtu awaye yote anayedhani kuwa kila taabu anayoipitia mtu ni kwa sababu aidha mtu huyo amefanya dhambi au wazazi wake, haya ndio yalikuwa mawazo ya wanafalsafa waliokwenda kumshauri na kumfariji Ayubu wao walikuwa na dhana inayoathiri wengi hata katika nyakati za leo, miongoni mwa watu wengi sana waliookoka leo wakiona mtu aliyeokoka anapatwa na mabaya wanadani kuwa mtu huyo ni mbaya au kuna dhambi ameifanya hajaitubia, au Mungu anashughulika naye anamuadhibu aina hii ya dhana ilikuwepo pia miongoni mwa wanafunzi wa Yesu na Yesu alikuwa tofauti na mtazamo wao? 

 

Yohana 9:1-3 “Hata alipokuwa akipita alimwona mtu, kipofu tangu kuzaliwa.  Wanafunzi wake wakamwuliza wakisema, Rabi, ni yupi aliyetenda dhambi, mtu huyu au wazazi wake, hata azaliwe kipofu? Yesu akajibu, Huyu hakutenda dhambi, wala wazazi wake; bali kazi za Mungu zidhihirishwe ndani yake.”

 

2.       Mtu anayefikiri kuwa kila mwanadamu anayeteseka anavuna alichokipanda – Ni ukweli ulio wazi kuwa maandiko yanazungumza juu ya kuwepo kwa kanuni ya kupanda na kuvuna

 

Wagalatia 6:7-9 “Msidanganyike, Mungu hadhihakiwi; kwa kuwa cho chote apandacho mtu, ndicho atakachovuna. Maana yeye apandaye kwa mwili wake, katika mwili wake atavuna uharibifu; bali yeye apandaye kwa Roho, katika Roho atavuna uzima wa milele. Tena tusichoke katika kutenda mema; maana tutavuna kwa wakati wake, tusipozimia roho.”

 

Wako watu duniani ambao wanadhani ya kuwa unapopita katika mapito Fulani basi ni kwa sababu ulipanda au kuna mtu kwenye ukoo wenu au baba zako alipanda ubaya Fulani na sasa unateseka kwa sababu unavuna au wewe ulifanya uovu Fulani na sasa unakujilia juu yako na wanaweza kumuhusisha Mungu katika jambo hilo kwamba Mungu analeta mabaya juu yako kwa sababu ya ubaya Fulani ulioutenda hii pia ilikuwa falsafa ya rafiki zake Ayubu walipokuja kumfariji, na watu wengi leo wana mtazamo kama huo wa KARMA lakini sio kila mapito yanatokana na Karma au mavuno Fulani.

 

3.       Mtu anayefikiri kuwa  wewe hufanikiwi au hupati muujiza kwa sababu huna Imani -  wako watu wengi sana ambao wakati mwingine wanaweza kuhukumu wenzao kuwa wewe hupati muujiza wako au Mungu hakufanyii jambo Fulani kwa sababu huna Imani, wakati wote wao wanafikiri tu kuwa Imani yao ndio imewasaidia kufikia hali waliyoifikia na wale wasio na imani wamebaki na michangamoto yao, falsafa na dhana ya namna hii pia inamuweka Mungu katika nafasi ya kufikiriwa kuwa anahusiana na wenye Imani pekee lakini maandiko yanamaanisha Imani ina pande mbili, na zote ni Imani.

 

Waebrania 11:35-39 “Wanawake walipokea wafu wao waliofufuliwa. Lakini wengine waliumizwa vibaya hata kuuawa, wasikubali ukombozi, ili wapate ufufuo ulio bora; wengine walijaribiwa kwa dhihaka na mapigo, naam, kwa mafungo, na kwa kutiwa gerezani; walipigwa kwa mawe, walikatwa kwa misumeno, walijaribiwa, waliuawa kwa upanga; walizunguka-zunguka wakivaa ngozi za kondoo na ngozi za mbuzi; walikuwa wahitaji, wakiteswa, wakitendwa mabaya; (watu ambao ulimwengu haukustahili kuwa nao), walikuwa wakizunguka-zunguka katika nyika na katika milima na katika mapango na katika mashimo ya nchi. Na watu hao wote wakiisha kushuhudiwa kwa sababu ya imani yao, hawakuipokea ahadi;”

 

Je watakatifu waliouawa kwaajili ya Imani, kina Stefano waliopigwa mawe na kufa kwaajili ya neno la uzima je walikuwa hawana Imani? Au Kristo mwenyewe mwenye haki aliyesulubiwa na kufa kifo kibaya msalabani je hakuwa na Imani?  Watakatifu waliopitia mateso na changamoto mbalimbali je walikuwa wamemkosea Mungu kuna haja ya kupanua mtazamo wako kuhusu changamoto mbalimbali wanazopitia watu wote duniani!

 

4.       Mfariji mwenye kutaabisha huzungumza zaidi ya kile anachokijua – Wafariji wengi wenye kutaabisha ni wepesi kuzungumza na ni wepesi kufikiri na kutoa maoni,  na sio wepesi kusikiliza, unaweza kuwa kwenye ndoa kama ya kwangu ina miaka 22 mimi ndio naishi na mke wangu, lakini kuna mtu anaweza kuja tu na kujifanya anatujua vizuri kuliko tunavyojijua kwa habari za kusikia tu, wafariji wenye kutaabisha hujifanya wanajua kila kitu, wanaweza kujifanya wanamjua mumeo kuliko wewe au wanamjua mkeo kuliko wewe au wanajua sana maisha yako au wana taarifa zako za miaka na siku nyingi au wanajua hata dhambi zako za zamani, hawajui kama ulitubu au la hawajui uhusiano wako na Mungu lakini wanaweza kujifanya wanajua na wakakizungumza kwa kujiamini na kwa uhakika kumbe wako mbali sana na mapenzi ya Mungu, Wako watu  wanaweza kujua hata kwanini unaugua figo, na wakawa na majibu yao, wanaweza kujua hata kwanini uliachishwa kazi na wakawa na majibu yao, wanaweza wakawa na jibu la kila kitu, Rafiki za Ayubu walikuwa na dhana kuwa dhambi inaleta changamoto za kila aina na haki inaleta thawabu na Baraka tele na mafanikio kwa hiyo hata kufa kwa watoto kumi wa Ayubu wao waliona kuwa huenda watoto hao walikuwa wamefanya dhambi na wakazungumza kwa uhakika ona

 

Ayubu 8:2-4 “Wewe utanena maneno haya hata lini? Maneno ya kinywa chako yatakuwa kama upepo mkuu hata lini? Je! Mungu hupotosha hukumu? Au, huyo Mwenyezi hupotosha yaliyo ya haki? Kwamba watoto wako wamemfanyia dhambi, Naye amewatia mkononi mwa kosa lao;”

 

Unaona Wafariji na washauri wa Ayubu walimwambia kuwa Mungu amewaua watoto wako kwa sababu walikuwa wamemfanyia Mungu dhambi na Mungu amewashughulikia kwaajili ya makossa yao! Wafariji wenye kutaabisha kwa ujumla huwa hawajui hata wanayoyazungumza, wao wanazungumza kwa uzoefu wa falsafa za dunia na hawawezi kuingia kwenye mashauri ya Mungu na kujua Mungu alikuwa anamaanisha nini na kwanini mambo yanatokea katika namna yanayotokea, lakini pia walikuwa wanadhani tu kwa kuunganisha mambo, na badala ya kumfariji Ayubu katika mapito yake walimuhukumu yeye na familia yake ! na badala ya kumpunguzia Msiba wake waliongeza huzuni zake!

 

5.       Mtu anayefikiri kuwa kikombe chako kimejaa  -  Kwamba Mungu huwa anahifadhi maovu anaandika mahali anakuangaliaaaaa afu kuna mstari mwekundu, kuna kikombe chako mahali siku kikijaaa sasa hasira zake zinawaka na anaanza kukushughulikia hii ni dhana ambayo imejengeka sana kwa watu wa Mungu kama wanajadili jambo kuhusu mapito yako wanaweza kusikika  na kusema aaa jamaa bhana kikombe chake kimejaa!:,  Hata sijui imeandikwa wapi au iko eneo gani katika maandiko ambapo Mungu emeeleza kuwa kuna matone ya dhambi yanaingia afu kikombe chako kikijaa anakushughulikia! Yaani tunaye baba Mbinguni ambaye anavizia maovu yetu yafikie kiwango Fulani alafu anamwaga mihasira yake ahaaaa ee kikombe kimejaa yaani kuna mambo kadhaa ulikuwa huyafanyi sasa Mungu ndio anashughulikna na wewe ulikuwa hutoi zaka, uliwaabisha wengine, uliwanyima chakula wenye njaa, hukuwajali wajane, hukuwajali yatima, hukwenda kuona wafungwa, uliwanyima maji wenye kiu, ulipendelea watu, uliwapuuzia yatima na wajane, ulikuwa na hiki ama kile kwa hiyo baada ya mlolongo huo mkubwa Mungu alikuwa anakucheki tu sasa kikombe kimejaa anakushughulikia ahaaa ona  dhana kama hii ilikuwa katika mioyo ya wafariji wa Ayubu waliokuja kumfariji na kumshauri n ahata leo wako watu wenye mitazamo kama hiyo

 

Ayubu 22::5-10 “Je! Uovu wako si mkuu? Wala maovu yako hayana mwisho. Kwa kuwa umetwaa dhamana kwa nduguyo bure, Na kuwavua nguo zao walio uchi. Hukumpa maji ya kunywa huyo aliyechoka, Nawe umemnyima chakula huyo mwenye njaa. Lakini huyo shujaa, nchi ilikuwa yake; Na huyo mwenye kusifiwa, yeye aliikaa. Umewafukuza wanawake wajane hali ya utupu, Na mikono ya mayatima imevunjwa. Kwa hiyo umezungukwa na mitego, Na hofu ya ghafula yakutaabisha,”

 

6.       Wafariji wenye kutaabisha hujiweka katika nafasi ya Mungu kuhukumu -  wakati ukiwa katika changamoto mbalimbali za maisha saa ya kujaribiwa kwako wafariji wenye kutaabisha hujisahau na kukaa katika nafasi ya Mungu  wakijifanya kuamua hatima ya maisha yako, au wakitaka kumsaidia Mungu kukuonjesha machungu zaidi, kumbe badala yake wanamkosea Mungu, waliokuja kumfariji Ayubu wote walihukumiwa na Mungu na ukweli ni kuwa Mungu alikasirishwa nao sana kwa kuwa hawakuwa sahihi kwa jinsi na namna walivyoshughulika na Ayubu

 

Ayubu 42:7-10 “Basi ikawa, baada ya Bwana kumwambia Ayubu maneno hayo, Bwana akamwambia huyo Elifazi Mtemani, Hasira zangu zinawaka juu yako, na juu ya hao rafiki zako wawili; kwa kuwa ninyi hamkunena yaliyo sawa katika habari zangu, kama alivyonena mtumishi wangu Ayubu. Basi sasa, jitwalieni ng'ombe waume saba, na kondoo waume saba, mkamwendee mtumishi wangu Ayubu, mjisongezee sadaka ya kuteketezwa; na huyo mtumishi wangu Ayubu atawaombea ninyi; kwa kuwa nitamridhia yeye, nisiwatende sawasawa na upumbavu wenu; kwani ninyi hamkunena maneno yaliyonyoka katika habari zangu, kama alivyonena mtumishi wangu Ayubu. Basi Elifazi, Mtemani, na Bildadi, Mshuhi, na Sofari, Mnaamathi, wakaenda, wakafanya kama vile Bwana alivyowaamuru; naye Bwana akamridhia Ayubu. Kisha Bwana akaugeuza uteka wa Ayubu, hapo alipowaombea rafiki zake; Bwana naye akampa Ayubu mara mbili kuliko hayo aliyokuwa nayo kwanza.”

 

Wafariji hawa walikosea hawakusema sawasawa kwa habari ya Mungu wala kwa habari za mtumishi wake Ayubu, na hivyo walikuwa na hatia walipata dhambi ambayo ilihitaji tena watoe dhabihu kisha waombewe na Ayubu ili Mungu aweze kuwarehemu! Je unapenda sana kujishaua shaua na kuingilia mambo ya watu katika maisha yao? Je unadhani uko sahihi kila wakati unaponena neno juu ya Masihi wa Bwana na mapito yake?  Je unadhani uko salama unapoongezea mateso juu ya watu wa Mungu, Je unadhani uko sahihi wakati wote unapojifanya unatoa ushauri kuhusu maisha na huduma ya Mtu wa Mungu? Je wewe ndio Mungu je wewe ndiye uliyemuita, je wewe ndio unajua anakokokwenda?  Je wewe unajifanya una uelewa mkubwa sana wa neno la Mungu kuliko mtu anayepitia mateso? Je wewe kwenye raha zako unadhani una ukaribu na Mungu kuliko mtu anayepitia kwenye mateso? Au mtu aliyevunjika moyo?  Wengi wa watu wanaojifanya wafariji, au washauri ndio wanaoharibu maisha ya watu zaidi na kumkosea Mungu kuliko unavyodhani kwa msingi huo lazima kila mmoja achukue tahadhari na kuacha kuingilia mapito na njia za mtu, tuwe marafiki tu, tuombeane tu lakini huna mamlaka ya kuingilia na kumuamulia mtu mpango wa Mungu alioukusudia kwa watu wake na maisha yake na mapito yake, Mungu akulinde wewe na mimi ili tusiwe miongoni mwa watu watakaokuwa wafariji wenye kutaabisha

 

Namna ya kujiepusha na wafariji wenye kutaabisha au kuwa wafariji wenye kutaabisha

1.       Acha kumuwazia Mungu kwa upumbavu!

 

Ni vizuri kukaa kimya wakati changamoto zinapozuka katika maisha yetu na kuacha kabisa kumuwazia Mungu kwa upumbavu, hakuna jambo linaweza kuhatarisha maisha yetu kama kukimbilia kuzungumza mambo kana kwamba tunajua sana, duniani kuna watu ni wajuaji kila kitu wanadhani wanakijua na wana majibu ya kila kitu, maandiko yanatufundisha kuwa ni vizuri kukaa kimya na kujichunga sana tunapozungumza mambo na zaidi pia tunaloliwaza kuhusu Mungu.

 

Ayubu 1:20-22 “Ndipo Ayubu akainuka, akalirarua joho lake, kisha akanyoa kichwa chake, na kuanguka chini, na kusujudia; akasema, Mimi nilitoka tumboni mwa mama yangu nili uchi, nami nitarudi tena huko uchi vilevile; Bwana alitoa, na Bwana ametwaa; jina la Bwana na libarikiwe. Katika mambo hayo yote Ayubu hakufanya dhambi, wala hakumwazia Mungu kwa upumbavu.”

 

Kufikiri kuwa kila mwanadamua aneyeteseka duniani ni kwa sababu ametenda dhambi ni kumwazia Mungu kwa upumbavu, hivi wewe ni mkamilifu kiasi ya kwamba Mungu anakuacha? Kama Mungu anagekuwa anamtesa kila mtu kwa sababu ya dhambi basi wanadamu wote wangekuwa walelazwa kwa mateso na magonjwa kutokana na uovu tulio nao maandiko yanaonyesha kuwa watu wote wamefanya dhambi na hakuna mwenye haki hata mmoja wala hakuna anayemtafuta Mungu Ayubu anatajwa kuwa alikuwa Mcha Mungu

 

Warumi 3:10-12 “kama ilivyoandikwa, ya kwamba, Hakuna mwenye haki hata mmoja. Hakuna afahamuye; Hakuna amtafutaye Mungu. Wote wamepotoka, wameoza wote pia; Hakuna mtenda mema, la! Hata mmoja.”

 

Kama unataka kuwa mshauri mzuri na mfariji mzuri uwe na uwezo mkubwa wa kulijua neno la Mungu na kumjua Mungu, na kuyajua mapenzi yake na njia zake, huwezi kuwa mfariji sahihi kama humjui Mungu wala neno lake na tabia zake na njia zake, tukilijua neno vema na tabia za Mungu na mapenzi yake tunaweza kufaa kuwa wafariji wazuri kwa kuwa tutawaelekeza watu katika kumuamini Mungu na kuwatia moyo wanapopitia katika changamoto mbali mbali, Mungu hana mahali ambapo anaweka rekodi ya uovu na kusubiri kikombe kijae, wala alishasema watoti hawatateseka kwa sababu ya dhambi za baba zao

 

 Zaburi 130:3-4 “Bwana, kama Wewe ungehesabu maovu, Ee Bwana, nani angesimama? Lakini kwako kuna msamaha, Ili Wewe uogopwe.”

 

Ezekiel 18:20 “Roho itendayo dhambi, ndiyo itakayokufa; mwana hatauchukua uovu wa baba yake, wala baba hatauchukua uovu wa mwanawe, haki yake mwenye haki itakuwa juu yake, na uovu wake mwenye uovu utakuwa juu yake.”

 

2.       Usiwe na majibu ya suluhisho la tatizo moyoni mwako

Marafiki wa Ayubu walifanya mambo mazuri kama matatu hivi waliposikia kuwa Ayubu amepatwa na majanga walimtembelea ni tofauti kidogo na nyakati za leo ambapo watu hukukimbia kama walivyomkimbia watu wengine, pili walilia kwa sauti kuu na kurarua mavazi yao kuonyesha kuwa waliguswa na changamoto alizopitia jamaa yao  na mwisho walikaa pamoja naye tena walikaa kimya kwa siku saba.

Tatizo lao ni kuwa hawakuweza kukaa kimya walikuwa na tafasiri yao kuhusu mateso yaliyompata Ayubu na walikuwa wanamtaka atubu ili kwamba Mungu aweze kumsamehe na kumbariki tena hii ilikuwa ushauri na suluhisho, nimeshakutana na watu wengi sana ambao unapokutana na changamoto wao wanakuambia UTUBU ni kana kwamba wewe kuna makosa Fulani makubwaaa umemfanyia Mungu na ndio maana unapitia hali unayoipitia, wanadhani kuwa sifahamu umuhimu wa toba wanadhani labda ninajihesabia haki kama ilivyo kwa Ayubu maandiko yalionyesha wazi kuwa Ayubu alikuwa safi, na Mungu mwenyewe alikuwa amejivunia kuhusu Ayubu na Shetani pia alikiri kuwa Ayubu alikuwa mwadilifu, kwa msingi huo basi ni wazi kuwa mapito ya Ayubu hayakuwa na uhusiano wowote na tabia zake, aidha wako watu ambao ukikosea wanataka kuona unaadhibiwa na Mungu na unapitia mambo magumu hata adhabu wanatoa wao haya ni makosa makubwa sana ya kitheolojia na ujuzi hafifu kuhusu Mungu, na neno lake, Mungu ni mwema na huwapa jua lake na mvua yake wema na waovu,  linapokuja swala la mapito huwa halichagui

Ayubu 2:9-10 “Ndipo mkewe akamwambia, Je! Wewe hata sasa washikamana na utimilifu wako? Umkufuru Mungu, ukafe. Lakini yeye akamwambia, Wewe wanena kama mmoja wa hao wanawake wapumbavu anenavyo. Je! Tupate mema mkononi mwa Mungu, nasi tusipate na mabaya? Katika mambo hayo yote Ayubu hakufanya dhambi kwa midomo yake.”     

Hatupaswi kuhisi tu kuwa mtu Fulani anapitia hali Fulani kwa sababu Fulani kwani kufanya hivyo pia ni kuingilia UBWANA wa Mungu, na hili ndio sababu iliyopelekea Mungu akawakemea Rafiki za Ayubu

3.       Zingatia kanuni za ushauri au kufariji

Ziko kanuni ambazo mfariji anapaswa kuzizingatia anapokwenda kumfariji mtu na kumshauri ikiwa ni pamoja na kuvaa kiatu na yeye aliyepatwa na majanga Warumi 12:15 “Furahini pamoja nao wafurahio; lieni pamoja nao waliao.” Kila mfariji lazima awe na uelewa wa kutosha kuhusu mapito na njia za Mungu, achana kabisa na mitazamo yenye kuhukumu achana nayo, hakikisha unakuwa na usiri na sio kutangaza siri za Muhusika, zingatia tamaduni za wahusika, acha kwenda kuwasanifu, watie moyo unaowafariji sawa sawa na mtazamo wao au wa neno la Mungu na mapenzi ya Mungu, waunge mkono isipikuwa tu kama fikira zao haziko sawa na Mapenzi ya Mungu, hakikisha unamjua Mungu vizuri na njia zake, kumbuka kuna wanaopatwa na ubaya kwa sababu ya mabaya lakini si kila anayepatwa na mabaya ni mbaya, Panua mtazamo wako wa kitheolojia na upana wa mapito katika mtazamo wa Mungu, Inua macho yako na kuchukua tahadhari kuhusu wema wa Mungu.

Hitimisho:

Hatuna budi kumuomba Mungu ili siku zote tuweze kuwa marafiki wazuri, wafariji wasioleta misiba, na washauri wenye weledi ili kwamba wale wote wanaopitia mapito ya aina mbalimbali na huzuni na magumu na maumivu tuweze kujua namna ya kuwatia moyo katika Mungu, wakati mwingine kama hatuna ufumbuzi wa jambo ni vema kukaa kimya usijitie kimbelembele kama mzungumzaji, Tumuombe Mungu atusaidie kama tunataka kusema tuseme yaliyo kweli na yale tunayoyajua na yaliyoko kwenye mapenzi yake, kama watu wana dhambi tuwaongoze kwenye mema, tuwe wafariji wenye haki, na sio wafariji wenye kutaabisha.

Na Rev. Innocent Mkombozi Kamote

Mkuu wa Wajenzi mwenye Hekima!

Jumanne, 7 Novemba 2023

Nafsi iliyoshiba taabu!


Zaburi 88:3-5 “Maana nafsi yangu imeshiba taabu, Na uhai wangu umekaribia kuzimu. Nimehesabiwa pamoja nao washukao shimoni; Nimekuwa kama mtu asiye na msaada. Miongoni mwao waliokufa nimetupwa, Kama waliouawa walalao makaburini. Hao ambao Wewe huwakumbuki tena, Wametengwa mbali na mkono wako.”



Utangulizi:

Mwandishi wa zaburi anazungumza maneno magumu sana kuelekea kwa Mungu Muumba, ni haki yake na ni haki ya watu wasiomjua Mungu na wanaomjua Mungu kusema maneno mazito kwa Muumba pale yanapokuwa yametukuta, Si kuwa mwandishi hakuwa mtu mwenye tumaini kwa Mungu hapana lakini alikuwa ni mtu aliyekata tamaa sana AMESHIBA TAABU na maisha yake yako hatarini kiasi ambacho ni kaburi tu ndio analoliona linamkabili, anajina amehesabiwa kama watu waliokufa tayari ingawa bado yuko hai, hana msaada, na anajiona kama ni miongoni mwa wafu basi yeye ni mfu aliyetupwa hana thamani hata ya kuzikwa, sawa tu na watu waliolala kaburini na wamesahaulika, sio na wanadamu tu hata Mungu ni kama hawakumbuki tena nje, mbali kabisa na uwepo wa Mungu, hali kama hii inawakuta wanadamu wote walioko duniani bila kujali una haki au hauna haki, unamcha Mungu au la, lakini tuwapo safarini hapa duniani sio kila jambo linaweza kuwa rahisi, wakati mwingine tunaweza kuwa na majanga mpaka nafsi zetu zikashiba taabu nini maana ya nafsi iliyoshiba taabu? Hilo ndio jambo la msingi tutakwenda kuliangalia katika somo hili !

Nafsi iliyoshiba taabu maana yake ni nafsi iliyoelemewa na hisia kali na za ndani sana za maumivu yanayopelekea mtu ajione kuwa hana matumaini tena ya kuishi, au kama mtu ambaye hawezi tena kupata msaada wowote kutoka kwa yeyote hapa duniani, unahisi uko mwenyewe na umekataliwa na huwezi kuunganishwa tena na yeyote, huwezi kushaurika na yeyote, huwezi kutiwa moyo na yeyote zaidi ya magumu yanayokukabili tu, kuwa katika hali ya nafsi kuugua, kuteseka, kusononeka na kuhuzunika au kushiba taabu kunakuweka katika nafasi ya kuhisi kuwa uko mwenyewe na hata wale uliowategemea wamekuacha ! na unachokiona katika maisha yako ni mauti tu ni kifo pekee ndicho kinachokukabili, huoni tumaini lolote unaona giza, heri hata wewe unaweza hata kusoma maandiko na au hata kufuatilia somo kama hili lakini nafsi iliyoshiba taabu huwa inajawa na huzuni nyingi kiasi cha kufa ona :-

Mathayo 26:37-39. “Akamchukua Petro na wale wana wawili wa Zebedayo, akaanza kuhuzunika na kusononeka. Ndipo akawaambia, Roho yangu ina huzuni nyingi kiasi cha kufa; kaeni hapa, mkeshe pamoja nami. Akaendelea mbele kidogo, akaanguka kifulifuli, akaomba, akisema, Baba yangu, ikiwezekana, kikombe hiki kiniepuke; walakini si kama nitakavyo mimi, bali kama utakavyo wewe.”

Je hali kama hiyo imewahi kukutokea? Watumishi wengi wa Mungu wanakutana na hali kama hiyo, Bwana wetu Yesu Kristo alikutana na hali kama hii alipokuwa akiukabili Msalaba alihitaji msaada hata wa rafiki zake lakini walilala, alitamani hata wangekesha na kuomba kwaajili yake lakini hawakuweza hawakuweza kumsaidia kwa sala wala hata kwa maombi wala ushauri! Yeye alimuomba Mungu na ni malaika wa Bwana tu waliokuja kumtia nguvu, Lakini afadhali hata Yesu alitiwa nguvu na malaika wa Bwana, Lakini mwandishi wa zaburi yeye hakukuwa na mawasiliano ya aina yoyote na mbingu.

Tuwapo duniani tunaweza kukutana na changamoto na mapito magumu sana kiasi cha kutufikisha katika hali kama hii, uwe mtu unayemuamini Mungu au hata usiyemuamini Mungu, kuna vipindi ambavyo unaweza kukutana navyo vikakujaza huzuni kiasi cha nafsi yako kushiba, na ukakosa majibu na kuanza kumlilia Mungu, kwanini mimi? Kwanini mimi eee Bwana! Mungu wangu mbona mimi tuuuu!. Hivi Mungu yupo kweli jamani, hivi Mungu anaona, hivi huyu muumba aweza kweli kutoa haki katika hili? Tunaweza kulia na kufikia ngazi ya kufikiri kuwa ni Mungu ameamua kututaabisha ametutupa!, asante katika agano jipya angalau tuna ufunuo kuwa shetani yupo na tunaweza kufikiri kuwa changamoto nyingine zinasababishwa nay eye, Lakini nyakati za agano la kale hawakujua sana habari za shetani na hivyo Mungu tu alibeba lawama zote!  Ona:-

Zaburi 88:14-16 “Bwana, kwa nini kuitupa nafsi yangu, Na kunificha uso wako? Nateswa mimi hali ya kufa tangu ujana, Nimevumilia vitisho vyako na kufadhaika. Hasira zako kali zimepita juu yangu, Maogofyo yako yameniangamiza.”  

Unaona mwandishi wa zaburi hii alifikia hatua ya kufikiri Mungu amemtupa, Mungu ameficha uso wake, na aliona ni kama maisha yake yanapita katika hasira kali za Mungu na akachoka, huenda nawe msomaji na msikilizaji wangu unapitia hali kama hii, Nafsi yako imeshiba taabu, hakuna wa kukujali, uzito wa hali yako ni kama hakuna anayehisi, uko ulimwenguni kama umefutwa tu, Lakini ashukuriwe Mungu wetu ni Mungu anayejali, yeye hamtupi mtu na Bwana anataka kuinua nafsi yako kupitia ujumbe huu, Bwana akupe neema ya kufuatilia somo hili kwa kina ili tuweze kupata suluhu, nafsi zetu zikaponywe na kuacha kufadhaika katika jina la Yesu, Amen! Tutajifunza somo hili kwa kuzingatia vipengele vitatu vifuatavyo:-

 

·         Maana ya nafsi iliyoshiba taabu!

·         Nafsi iliyoshiba taabu.

·         Mambo ya kufanya Nafsi inaposhiba taabu.

 

Maana ya nafsi iliyoshiba taabu.

Nafsi iliyoshiba taabu kama nilivyogusia kwenye utangulizi ni nafsi iliyoelemewa na hisia kali na za ndani sana za maumivu yanayopelekea mtu ajione kuwa hana matumaini tena ya kuishi, Na mwandishi wa zaburi anaonyesha kuwa alikuwa katika taabu iliyopitiliza kiasi cha kukata tamaa au kiasi cha kufa mwenyewe anasema MAANA NAFSI YANGU IMEJAA TAABU neno taabu linalotumika hapo katika lugha ya Kiebrania linatumika neno RAAH ambalo limetajwa katika maandiko mara 663  na kwa kiyunani ni PERILUPOS  ambalo tafasiri yake kwa kiingereza ni EXCEEDING SORROWFUL au AGONY ambalo maana yake kwa kiingereza ni Extreme physical, mental, and psychological suffering  yaani kwa lugha yetu ni Hatua ya juu na ya mwisho kabisa katika maumivu ya mwili, akili na nafsi kuelekea kufa ni huzuni ya kupita kawaida ni kuugua kwa ndani kabisa kama ingetokea mtu ni mgojwa wa mwili tungeweza kusema kuwa yuko mahututi!

Sa katika maisha haya ya dunia hii iliyojaa taabu kwa kawaida ziko taabu ambazo tunaweza kuvumilia lakini inapofikia hatua ya kushiba taabu, maana yake mtu amefikia hatua ya mwisho kabisa ya kuvumilia taabu hizo na anatamani katika akili yake afe! Yaani ni mtu aliyehemewa na kukata tamaa na amezidiwa amelemewa ametaabika kiasi cha kuona kifo ndio suluhu ya changamoto yake Nafsi inaposhiba taabu huwezi kamwe kuhisi uwepo wa Mungu, unakuwa tu na hisia kuwa Mungu amekutelekeza na kama unamcha Mungu unafikia ngazi ya kuchanganyikiwa kwamba Mungu anawezaje kuachilia hali ngumu na nzito kama hii? ukweli ni kwamba rafiki yako wa karibu anakuwa ni giza tu na unapoteza uwezo wa kufikiria kuwa utaokolewa, hata wanaojaribu kukutia moyo unaweza kushangazwa na Imani yao kwani wewe unaona tu yasiyowezekana kwa ujumla hakuna jambo baya duniani kama kuwa na nafsi iliyoshiba taabu, watu wengi wanaojiua ni wale ambao nafsi zao zilijaa taabu na wakakosa msaada au hata watu wa kuwatia moyo hii ni hali ngumu sana duniani

Mwandishi wa zaburi hii anaonyesha kuwa alikuwa amefikia kiwango cha juu kabisa cha taabu na huzuni na katika zaburi zinazoonyesha kiwango cha huzuni hii ni zaburi ya juu  zaidi katika zaburi zote zenye hisia kali za kuelemewa jambo kubwa la msingi ni kuwa zaburi hii imeandikwa kutundisha ya kuwa Mungu hawezi kuatuacha hata kama tunapita katika hali ngumu kwa kiasi gani  kama tunamtegemea yeye ni lazima atafanya njia na kutuokoa watoto wake bila kujali hali zetu

Kumbukumbu 31:6 “Iweni hodari na moyo wa ushujaa, msiogope wala msiwahofu; kwa maana Bwana, Mungu wako, yeye ndiye anayekwenda pamoja nawe, hatakupungukia wala kukuacha.”

Waebrania 13:5 “Msiwe na tabia ya kupenda fedha; mwe radhi na vitu mlivyo navyo; kwa kuwa yeye mwenyewe amesema, Sitakupungukia kabisa, wala sitakuacha kabisa.”

Mungu hatakuacha katika hali yoyote ngumu endapo utaliitia jina lake, huyu ni baba anayejali, anayeona, anayefuatilia, anayefundisha na anayetuwazia mema hata katika mazingira yasiyo na matumaini, Mwandishi wa nyimbo za injili namba 122 anasema umechoka umeshushwa moyo, mwambie Yesu, wote tunajua kuwa tukimwambia Yesu hataweza kutuacha atashughulika nasi.

Nafsi iliyoshiba taabu.

Maisha sio kila wakati yana weza kuwa ya furaha, mateso na kupoteza ni moja ya fungu la maisha ya mwanadamu, Hata watu waliojitoa kwa Mungu na kutumiwa na Mungu kwa kiasi kikubwa walikutwa na maisha ya taabu wakati Fulani, mwandishi wa zaburi hii alikuwa katika kilele cha juu zaidi cha taabu yake, kwa kawaida kila mwanadamu kwa kiwango chake anapofikia katika kiwango cha kuwa na huzuni yajuu kabisa au nafsi yake kushiba taabu haoni nuru tena, anaona giza, haoni faida ya siku yake ya kuzaliwa na kilele cha juu kabisa cha suluhisho lake huona ni kifo, Kuwa na uhusiano mzuri au mbaya na Mungu sio sababu hata kidogo ya kukufanya usikutane na taabu, asili ya taabu na masumbufu ya maisha haya ni anguko la Mwanadamu, Tangu Adamu na Eva wazazi wetu walipoasi walifungua mlango wa kifo, mlango wa kifo hutafuta kuua kila kitu katika maisha yetu, kila kitu kina pigwa vita ya mauti, tangu unazaliwa, masomo yako, malezi yako, maisha yako, biashara zako, ndoa yako, kazini kwako, familia yako, mke wako, mume wako, watoto wako,  mazingira yako, chakula chako, biashara zako, kanisa lako na chochote kile kwa namna yoyote ile vitatafuta kupingana nawe na ndipo tunapojikuta tuko katika mazingira ya taabu, “Niliwahi kumwambia mke wangu hivi laiti ingekuwa maisha yanasomewa kwanza kisha ukihitimu ndio unaishi, basi watu wengi tungechagua kutokuzaliwa na kuishi duniani nadhani nikiwamo mimi!”, Lakini kwa bahati mbaya au njema maisha ni zawadi ambayo hatukuichagua, lakini ni zawadi ya thamani na hivyo kama tumepewa ni lazima tukubali kupambana na kila linalotukabili kwaajili ya utukufu wa Mungu,

Yakobo maisha yake yalijaa taabu alipoulizwa una miaka mingapi jibu lake lilikuwa refu kuliko swali lenyewe 

Mwanzo 47:7-9 “Yusufu akamleta Yakobo babaye ndani akamweka mbele ya Farao Yakobo akambariki Farao. Farao akamwuliza Yakobo, Je! Siku za miaka ya maisha yako ni ngapi? Yakobo akamjibu Farao, Siku za miaka ya kusafiri kwangu ni mia na thelathini; siku za miaka ya maisha yangu zimekuwa chache, tena za taabu, wala hazikufikilia siku za miaka ya maisha ya baba zangu katika siku za kusafiri kwao.”

Unaona huyu ni Mtumishi wa Mungu, Yakobo au Israel, anapoulizwa swali kuhusu maisha anajibu hapa akiwa na miaka 130 anaonyesha kuwa afadhali siku za baba zake wao waliishi sana na changamoto hazikuwa kubwa lakini yeye maisha yake YALIJAA TAABU, kwa lugha nyingine alishiba taabu, Neno taabu lililotumika hapo ni neno la Kiebrania RAAH, yaani mbaya, za taabu, za shida, za maumivu, za mateso, za kukatisha tamaa, zisizopendeza, zenye msongo wa mawazo, zenye huzuni, nzito, ngumu, sio za kupendeza, mbaya sana, njaatupu, za hovyo, za kilio, za masononeko, za vitisho, za misiba, za majanga, za bahati mbaya, zisizofaa, zenye madhara, hatarishi, huo ndio ufafanuzi wa neno hilo RAAH yaani kuhuzunisha kupita kawaida unaona

Akieleza kuhusu maisha Ayubu anasema katika kitabu chake Ayubu 14:1 “Mwanadamu aliyezaliwa na mwanamke Siku zake za kuishi si nyingi, naye hujaa taabu.” Unaona Ayubu anatumia neno HUJAA TAABU kwa lugha ya Kiebrania kumetumika neno ROGEZ linalotamkwa ROGHEZ akimaanisha siku za maisha ya Mwanadamu hazina starehe, hazina utulivu, zinatisha, ni za hasira

Unajua Ayubu alikuwa Mcha Mungu aliishi maisha matakatifu, alikuwa kuhani wa Mungu wa ngazi yajuu sana, lakini hilo haliwezi kuwa sababu ya kutokuonja taabu naye maisha yake unafahamu nafsi yake ilishiba taabu anasehema ni kama mwanadamu anazaliwa ili akutane na mashaka tu

Ayubu 5:7-11 “Lakini mwanadamu huzaliwa ili apate mashaka, Kama cheche za moto zirukavyo juu. Lakini mimi ningemtafuta Mungu, Ningemwekea Mungu daawa yangu; Yeye afanyaye mambo makuu, yasiyotambulikana; Mambo ya ajabu yasiyo na hesabu; Yeye atoaye mvua inyeshe juu ya nchi, Na kuyapeleka maji mashambani; Awainuaye juu hao walio chini; Na hao waombolezao hukuzwa wawe salama.”

Unaona Bahati nzuri yeye anasema atamchagua Mung utu anapopita katika hali ngumu, wengine kwa sababu ya nafsi kutaabika na kukosa matumaini ndipo wanapoamua kwenda kwa waganga, na wachawi kutafuta msaada, wakati nafsi inapotaabika mtihani wa moyo unapita kupima kuwa utamwangalia nani?

               

 

jambo kubwa zaidi la kumshukuru Mungu mwandishi wa zaburi 88 hakuwahi kutaka kujiua, wala kuwaendea waganga,  lakini alikuwa anaona kuwa Mungu ana wajibika na taabu zote anazozipitia na kuwa ni yeye Mungu ambaye hajajibu maombi yake, wakati nafsi yake imekaribia kufa, Nafsi yake imeshiba taabu, na amekuwa kama mfu hata miongoni mwao waliokufa yeye ametupwa, ametengwa mbali na watu, watu wanamchukia, yupo kwenye kifungo asichoweza kutoka, na anaanza kuwa na shaka kama atamsifu Mungu na kusimulia matendo yake akiwa kaburini na inaonekana kuwa tangu ujana wake maisha yamejaa taabu tu  hii ndio hali ya mtu anapofikia ngazi ya nafsi kushiba taabu

Ndugu yangu nafsi yako inapojaa taabu wewe unakimbilia wapi? Nani anakuwa kuhani wako, je unadhani kujiua ndio suluhu? Je unadhani wewe ndio pekee unayapitia haya? Hapana wewe sio wa kwanza, wala wewe huko peke yako tofauti zetu ni kuwa wengine hawasimulii yanayowakuta lakini kila mwanadamu hata waliofanikiwa wakikuelezea wanayoyapitia utajua kuwa watu wengi wana nafsi zilizojaa taabu!

 

Mambo ya kufanya Nafsi inaposhiba taabu.

Najua kuwa umepitia changamoto ngumu sana na wako watu wamepitia hata mimi pia, kila mmoja anesema aelezee anayoyapitia nadhani kila mmoja sawa na mzani wake anaweza kukiri kuwa yeye ndiye mwanadamu aliyepitia changamoto nyingi zaidi kuliko mwingine, vyovyote iwavyo, masiha yangu pia yamekuwa na taabu zisizoweza kuelezeka, naweza kusema pia kama Yakobo nadhani ni afadhali ya siku za baba zangu, hata hivyo sijawahi kupungukiwa na wema wa Mungu, wakati wote nilipopoteza tumaini hata wakati wa mambo magumu sana, niliziona fadhili za Bwana hakika wema nza fadhili zake zinanifuata mimi siku zote za maisha yangu, nawe pia ndugu yangu Mungu hatapunguza wema wake kwako yeye atakupa kutoboa, na hatimaye ataandaa meza katikati ya watesi wako, nini unatakiwa kufanya wakati huu

1.       Mtumaini Mungu – Mithali 3:5-6 “Mtumaini Bwana kwa moyo wako wote, Wala usizitegemee akili zako mwenyewe; Katika njia zako zote mkiri yeye, Naye atayanyosha mapito yako.”

 

2.       Mkimbilie Mungu – Mwandishi wa zaburi 88 anaanza kwa kuliitia jina la Bwana hata pamoja na nafsi yake kushiba taabu hakuwaza kwenda kwa waganga na badala yake aliendelea kuliitia jina la Bwana kwaajili ya wokovu wake, Ni Yesu tu anayeweza kuwa jibu la taabu zetu zote Zaburi 46:1-3 “Mungu kwetu sisi ni kimbilio na nguvu, Msaada utakaoonekana tele wakati wa mateso.Kwa hiyo hatutaogopa ijapobadilika nchi, Ijapotetemeka milima moyoni mwa bahari. Maji yake yajapovuma na kuumuka, Ijapopepesuka milima kwa kiburi chake.”

 

3.       Ifundishe nafsi yako kuabudu – Wakati unapofikia ngazi ya kuzidiwa na taabu kwa kuwa ni nafsi ndiyo inayosumbuka nafsi hiyo useme nayo, uishirikishe kumuabudu Mungu, uishirikishe kukumbuka mambo kadhaa hata kama ni machache aliyoyafanya Mungu, ikumbushe nafsi isisahau kuwa na shukurani, ikumbushe nafsi matendo makuu ya Mungu

 

Zaburi 103:1-4 “Ee nafsi yangu, umhimidi Bwana. Naam, vyote vilivyo ndani yangu Vilihimidi jina lake takatifu. Ee nafsi yangu, umhimidi Bwana, Wala usizisahau fadhili zake zote. Akusamehe maovu yako yote, Akuponya magonjwa yako yote, Aukomboa uhai wako na kaburi, Akutia taji ya fadhili na rehema,”

 

4.       Usijiombee kufa – Maisha yetu ni zawadi, hatukuchagua kuzaliwa kwa hiyo unapokuwa katika wakati wa taabu ni rahisi kumshutumu Mungu na kumwambia inatosha niondoe HAPANA usiombe hivyo kuomba hivyo ni kukosa shukurani ni kumjibu Mungu kuwa ulituumba bure tu huna makusudi nasi, ni afadhali kujua kuwa taabu yako ina somo gani baada ya kumaliza na Mungu katika shule yake kuliko kujiombea kufa hata hivyo Mungu huwa hajibu dua za namna hiyo

 

-          Ayubu alijua kuwa baada ya moto wa taabu yake atatoka akiwa angaa zaidi kama dhahabu ona Ayubu 23:10-12 “Lakini yeye aijua njia niendeayo; Akisha kunijaribu, nitatoka kama dhahabu. Mguu wangu umeshikamana sana na hatua zake; Njia yake nimeishika, wala sikukengeuka. Sikurudi nyuma kuiacha amri ya midomo yake; Nimeyatunza maneno ya kinywa chake zaidi ya riziki yangu,”

 

-          Musa alijiombea kufa – alipozidiwa na majukumu na taabu za uongozi wa kuongoza watu wanaonung’unika Musa aliona taabu sana na akamuomba Mungu ikiwezekana afe ona Hesabu 11:4-15. “Kisha mkutano wa wafuasi waliokuwa kati yao, wakashikwa na tamaa; wana wa Israeli nao wakalia tena, wakasema, N'nani atakayetupa nyama tule? Twakumbuka samaki tuliokula huko Misri bure; na yale matango, na matikiti, na mboga, na vitunguu, na vitunguu saumu; lakini sasa roho zetu zimekauka; hapana kitu cho chote; hatuna kitu cha kutumaini isipokuwa hii mana tu. Na hiyo mana ilikuwa mfano wa chembe za mtama na kuonekana kwake kulikuwa kama kuonekana kwake bedola. Watu wakazunguka-zunguka na kuikusanya, kisha wakaisaga kwa mawe ya kusagia, au kuitwanga katika vinu, kisha wakaitokosa nyunguni, na kuandaa mikate; na tamu yake ilikuwa kama tamu ya mafuta mapya. Umande ulipoyaangukia marago wakati wa usiku, hiyo mana ilianguka pamoja nao. Basi Musa akawasikia watu wakilia katika jamaa zao zote, kila mtu mlangoni pa hema yake; na hasira za Bwana zikawaka sana; Musa naye akakasirika. Musa akamwambia Bwana, Mbona umenitenda uovu mimi mtumishi wako? Kwa nini sikupata neema machoni pako, hata ukanitwika mzigo wa watu hawa wote juu yangu? Je! Ni mimi niliyewatungisha mimba watu hawa wote je! Ni mimi niliyewazaa, hata ikawa wewe kuniambia, Haya, wachukue kifuani mwako, mfano wa baba mwenye kulea achukuavyo mtoto anyonyaye, uende nao mpaka nchi uliyowaapia baba zao? Nipate wapi nyama ya kuwapa watu hawa wote? Kwani wanililia, wakisema Tupe nyama, tupate kula. Mimi siwezi kuwachukua watu hawa wote peke yangu, kwa kuwa ni mzigo mzito sana wa kunishinda. Na kama ukinitenda hivi, nakuomba uniulie mbali, kwamba nimepata fadhili mbele ya macho yako; nami nisiyaone haya mashaka yangu.”  Ni hali ya kawaida wakati mtu anapokuwa katika taabu na nafsi yakle ikalemewa huwa hawazi kuhusu uweza wa Mungu na hivyo hufikiri kuwa suluhisho ni kufikia mwisho kuliko kuona aibu au uchungu ulioko mbele lakini Musa hakujua kuwa Mungu alikuwa na mpango mwema nasema hivi usikufe wala usiombe kufa kwa sababu Mungu anataka kutukuzwa katika njia unayoipitia           

 

-          Eliya – alikuwa nabii aliyeweza kufanya mambo makubwa sana lakini ulipokuja mtihani wa taabu alikata tamaa sana alitishiwa tu na malikia Yezebeli kuwa atamkata kichwa, Eliya alikimbia mbio aligoma hata kula na maombi yake yakawa anataka tu afe ona

 

1Wafalme 19: 2-4 “Ndipo Yezebeli akampelekea Eliya mjumbe, kusema, Miungu wanifanyie hivyo na kuzidi, nisipokufanya roho yako kesho, panapo wakati huu, kama roho ya mmojawapo wa hao. Naye alipoona hayo, aliondoka, akaenda aihifadhi roho yake, akafika Beer-sheba, mji wa Yuda, akamwacha mtumishi wake huko. Lakini yeye mwenyewe akaendelea katika jangwa mwendo wa siku moja, akaenda akaketi chini ya mretemu. Akajiombea roho yake afe, akasema, Yatosha; sasa, Ee Bwana, uiondoe roho yangu; kwa kuwa mimi si mwema kuliko baba zangu.”

 

Unaweza kumcheka Eliya ukisoma kisa kizima cha ushujaa wake na mkwara kutoka kwa mwanamke, lakini zingatia kila mwanadamu ana kiwango chake cha mwisho cha uvumilivu huyu alipotumiwa ujumbe tu kuwa kesho nitakuua naapa kwa miungu yangu, Tayari aliogopa na kukimbia na kugoma kula na kulalal chini ya mti akisubiri kufa, Mungu ndiye anayetoa maisha na ni mpaka kusudi lake litimie ndani yetu Mungu hakukubali ombi hili, n ahata kifo kiliahirishwa kwake, hivyo usijiombee kufa wala usiogope

 

5.       Usiogope – kila wakati wito wa Mungu katika maandiko unatutaka tusiogope hii ni kwa sababu Mungu yuko pamoja nasi hata katika wakati tukiwa na hisia za kuwa peke yetu Mungu ni Roho kuna wakati anaruhusu tuhisi uwepo wake hivyo hata miili yetu inahisi kuwa yuko pamoja nasi lakini kuna wakati hatoruhusu tumhisi, tunahitaji Imani wakati huo, tunahitaji kutupilia mbali hofu, tunahitaji kutembea katika shuhuda zake tu tuikijua kuwa yupo na anashughulika na maisha yetu hata kama tunaiona mauti kumbuka yupo!

 

Zaburi 23:1-6 “Bwana ndiye mchungaji wangu, Sitapungukiwa na kitu. Katika malisho ya majani mabichi hunilaza, Kando ya maji ya utulivu huniongoza. Hunihuisha nafsi yangu; na kuniongoza Katika njia za haki kwa ajili ya jina lake. Naam, nijapopita kati ya bonde la uvuli wa mauti, Sitaogopa mabaya; Kwa maana Wewe upo pamoja nami, Gongo lako na fimbo yako vyanifariji. Waandaa meza mbele yangu, Machoni pa watesi wangu. Umenipaka mafuta kichwani pangu, Na kikombe changu kinafurika. Hakika wema na fadhili zitanifuata Siku zote za maisha yangu; Nami nitakaa nyumbani mwa Bwana milele.”

 

Hitimisho:

 

Mungu hatakusaliti – Mwandishi wa zaburi hii ya 88 ni HERMAN Mwana wa KORAH huyu ndiye mwandishi wa zaburi hii ni zaburi miongoni mwa zaburi zilizokuwa zinaimbwa wakati watu wanapopanda kwenda Hekaluni zinaitwa zaburi za KUPANDIA hii ndio zaburi chungu zaidi kuliko zote wayahudi waliita zaburi ya GIZA iliimbwa kwa machozi na watu waliokuwa wanahitaji msaada wa Mungu wakiwa hawajui maisha yatakuwaje, wakiwa na maswali mengi yasiyo na majibu wakifikiri kuwa Mungu pia amewaacha HERMAN anatuwakilisha sisi wote tunaweza kulalamika nadhani mimi ni mlalamikaji zaidi kuliko hata ninyi wasomaji wangu, nampenda Mungu lakini wakati mwingine simuelewi anaponipitisha katika magumu namuona kama ameniacha namuona kama amenisaliti, HERMAN mimi na wewe msomaji wangu tunamuona kama Mungu ametusaliti, na rafiki yetu ni giza tu nafsi imetupwa, maombi hayajibiwi, wanaotujua wametuacha, fadhaa zimetujaa? Je umewahi kufikia hali kama hii? Herman mwandishi wa zaburi hii Mwana wa kora aliifikia akidhani Mungu amemsaliti,

 

Zaburi 88:14-18 “Bwana, kwa nini kuitupa nafsi yangu, Na kunificha uso wako? Nateswa mimi hali ya kufa tangu ujana, Nimevumilia vitisho vyako na kufadhaika. Hasira zako kali zimepita juu yangu, Maogofyo yako yameniangamiza. Yamenizunguka kama maji mchana kutwa, Yamenisonga yote pamoja. Mpenzi na rafiki umewatenga nami, Nao wanijuao wamo gizani.”

 

Mungu ni mwaminifu katika ahadi zake kwa vyovyote vila haitakuja itokee akuache na asijali kuhusu maisha yako na yangu yeye hataweza kutusaliti wala kutuacha gizani yuko pamoja nasi hata ukamilifu wa Dahari, atatutia nguvu, atatusaidia na atatushika mkono na kutuinua hii ni ahadi yake na ndivyo itakavyokuwa katika maisha yetu siku zote Amen

 

Isaya 41:10 . “usiogope, kwa maana mimi ni pamoja nawe; usifadhaike, kwa maana mimi ni Mungu wako; nitakutia nguvu, naam, nitakusaidia, naam, nitakushika kwa mkono wa kuume wa haki yangu.”

 

Na. Mkuu wa wajenzi mwenye Hekima

Rev. Innocent Mkombozi Kamote.