Jumapili, 22 Mei 2022

Kwa sababu hawawezi kuvumilia Baraka zako !


Mwanzo 26:12-22 “Isaka akapanda mbegu katika nchi ile, akapata mwaka ule vipimo mia kwa kimoja, BWANA akambariki. Na mtu huyu akawa mkuu, akazidi kusitawi, hata akawa mkuu sana. Akawa na mali ya kondoo, na mali ya ng'ombe, na watumwa wengi. Hao Wafilisti wakamhusudu. Na vile visima vyote walivyochimba watumwa wa baba yake, siku za Ibrahimu babaye, Wafilisti walikuwa wamevifukia, wakavijaza kifusi. Abimeleki akamwambia Isaka, Utoke kwetu, maana wewe una nguvu sana kuliko sisi. Basi Isaka akatoka huko akapiga kambi katika bonde la Gerari, akakaa huko.  Isaka akarudi akavichimbua vile visima vya maji walivyovichimba siku za Ibrahimu babaye; maana wale Wafilisti walikuwa wamevifukia baada ya kufa kwake Ibrahimu; naye akaviita majina kufuata majina alivyoviita babaye. Watumwa wa Isaka wakachimba katika lile bonde, wakapata kisima cha maji yanayobubujika. Wachungaji wa Gerari wakagombana na wachungaji wa Isaka wakisema, Maji haya ni yetu. Ndipo akakiita jina la kile kisima Eseki, kwa sababu waligombana naye. Wakachimba kisima kingine, wakagombania na hicho tena. Akakiita jina lake Sitna. Akaondoka huko akachimba kisima kingine, wala hicho hawakukigombania. Akakiita jina lake Rehobothi, akasema, Kwa kuwa sasa BWANA ametufanyia nafasi, nasi tutazidi katika nchi.”


 

Utangulizi:

Ni muhimu kufahamu kuwa katika ulimwengu tulionao ni watu wachache sana tena wenye ukomavu wa kifikra wanaoweza kustahimili pale mtu mwingine anapobarikiwa, na wako wengi wenye kushangaza katika upande wa pili ambao hawawezi kuvumilia pale Mungu anapokubariki, Baraka za Mungu kwetu zina tabia ya kuvutia umati mkubwa sana wa watu, lakini pia zinauwezo wa kuvutia maadui kwa upande mwingine, kwa msingi huo kila mmoja anapokuwa amebarikiwa na mbaraka wa Mungu na mbaraka huo ukamtajirisha ni lazima aelewe kuwa atakuwa na maadui na hawa ni wale ambao hawawezi kuvumilia Baraka zako na hivyo wakati mwingine tunaweza kujikuta tunavuna Baraka lakini tunapata na changamoto za Baraka hizo, kimsingi Mungu katika mapenzi yake kamili alikusudia kuwa Baraka zake zisilete huzuni iwayo yote ona Mithali 10:22 “Baraka ya Bwana hutajirisha, Wala hachanganyi huzuni nayo.”   Lakini kwa sababu tuko duniani wakati mwingine Baraka hizo zitaambatana na huzuni au udhia kutokana na watu wanaotuzunguka kushindwa kustahimili kishindo cha Baraka za Mungu kwetu, ni muhimu kufahamu kuwa watu wanaweza kushindwa kustahimili Baraka za Mungu kwetu katika mazingira yafuatayo-

1.       Wakati mwingine Mungu anapotutakabali.

Watu wengine wanaweza kushindwa kuvumilia Baraka zetu tunapotakabaliwa na Mungu, kutakabaliwa na Mungu katika lugha ya kiingereza ni “When God looked us with favor” ni tukio la kukubalika kiibada Mungu kukubali au kusikiliza maombi yetu na dua zetu, wengine wanachukizwa kwa nini huyu amesikilizwa na Mungu, kwanini huyu ameolewa mie bado, kwanini huyu amejenga mie bado, kwa nini huyu ana mashamba mimi bado, kwa nini huyu ana watoto mimi bado wako watu wanashindwa kuvumilia wanapoona Mungu amekutakabali, wanaweza kuona wivu, wanaweza kukukasirikia na wanaweza hata kukuua.

 

Mwanzo 4:1-8 “Adamu akamjua Hawa mkewe; naye akapata mimba, akamzaa Kaini, akasema, Nimepata mtoto mwanamume kwa BWANA.  Akaongeza akamzaa ndugu yake, Habili. Habili alikuwa mchunga kondoo, na Kaini alikuwa mkulima ardhi. Ikawa hatimaye Kaini akaleta mazao ya ardhi, sadaka kwa BWANA. Habili naye akaleta wazao wa kwanza wa wanyama wake na sehemu zilizonona za wanyama. BWANA akamtakabali Habili na sadaka yake; bali Kaini hakumtakabali, wala sadaka yake. Kaini akaghadhibika sana, uso wake ukakunjamana. BWANA akamwambia Kaini, Kwa nini una ghadhabu? Na kwa nini uso wako umekunjamana? Kama ukitenda vyema, hutapata kibali? Usipotenda vyema dhambi iko, inakuotea mlangoni, nayo inakutamani wewe, walakini yapasa uishinde. Kaini akamwambia Habili nduguye, [Twende uwandani] Ikawa walipokuwapo uwandani, Kaini akamwinukia Habili nduguye,akamwua.”

 

Habili alipoteza maisha kwa sababu ya kutakabaliwa na Mungu, kaini alijawa na wivu wenye uchungu na kumkusudia nduguye mabaya, unaweza kukusudiwa mabaya, unaweza kupigwa vita kwa sababu una huduma nzuri, unaweza kupigwa vita kwa sababu unahubiri vizuri, kwa sababu unaimba vizuri, kwa sababu una sura nzuri, kwa sababu uko vizuri katika kila eneo kwa nini inafanyika hivyo ni kwa sababu wako watu hawawezi kuvumilia Baraka zako!

               

2.       Wakati mwingine tunapopata kibali kuliko wao.

 

Watu wengine wanaweza kushindwa kuvumilia Baraka zako kwa sababu tu unakibali, unakubalika kuliko wao, kwa sababu ya wao kujiona duni “inferiority complex” kutokana na kukubalika kwako wataanza kukuchukia na kukuonea wivu na hata kukupiga vita kwanini kwa sababu hawawezi kuvumilia Baraka zako ona

 

Mwanzo 37:3-5 “Basi Israeli akampenda Yusufu kuliko wanawe wote, maana ni mwana wa uzee wake, akamfanyia kanzu ndefu. Ndugu zake wakaona ya kuwa baba yao anampenda kuliko ndugu zake wote, wakamchukia, wala hawakuweza kusema naye kwa amani. Yusufu akaota ndoto, akawapa ndugu zake habari, nao wakazidi kumchukia;”

 

Ndugu zake Yusufu walipoona kuwa Yusufu anapendwa zaidikuliko wao, na baba yake amemnunulia nguo nzuri anapiga pamba kali kuliko wao,  wanabadilishana mawazo na mzee Yakobo, Yusufu anatoa taarifa kwa baba yake kuhusu kila kitu nyumbani jamaa wakahisi anapendelewa walishindwa kuvumilia Baraka hii ya kibali na wakazidi kumchukia sana, wako watu wanaweza kuchukizwa nawe kwa wazi au mioyoni mwao na wakawa wanaumia tu kwa sababu wewe unapendwa, kwa sababu wewe una kibali, una kibali kazini, unakibali kwa bosi, una kibali kikubwa na ni Mungu amesababisha kibali hicho na wanaokuzunguka wakashindwa kuvumilia Baraka zako na wanaanza kuchukizwa nawe na kukuonea wivu kwa sababu hawawezi kuvumilia Baraka zako!

 

3.       Wakati mwingine tunapopewa sifa zaidi kuliko wao

 

Watu wengine wanaweza kushindwa kuvumilia Baraka zako kwa sababu tu umesifiwa kuliko wao unaupiga mwingi katika jamii kuwazidi, unaposifiwa zaidi au sana kuliko wao, wao wanaaza kujiona duni na kupoteza kujiamini na hivyo wanaweza kukuonea wivu na kujenga uadui na kuanza kukupiga vita tangu waliposikia sifa zako kwanini watafanya hivyo kwa sababu hawawezi kuvumilia Baraka zako!

1Samuel 18:6-9 “Hata ikawa, walipokuwa wakienda, hapo Daudi aliporudi baada ya kumwua yule Mfilisti, wanawake wakatoka katika miji yote ya Israeli, kwa kuimba na kucheza, ili kumlaki mfalme Sauli; wakatoka na matari, na shangwe, na vinanda. Nao wale wanawake wakaitikiana wakicheza, wakasema, Sauli amewaua elfu zake, Na Daudi makumi elfu yake. Basi Sauli akaghadhibika sana, na maneno haya yakamchukiza; akasema, Wamempa Daudi makumi elfu, na mimi wamenipa elfu tu; kuna nini tena awezayo kupata, isipokuwa ni ufalme? Sauli akamwonea Daudi wivu tangu siku ile     

 

Unaona ni Daudi ambaye kwa nia njema alikuja kumpiga Goliath ambaye alikuwa ni adui wa taifa zima alisumbua ati kwa hiyo shujaa wa wafilisti alipigwa na Daudi ambaye ndani yake kulikuwa na upako wa kiungu ambao ulimwezesha kuwatetea wana wa Israel na jina la Mungu likatukuzwa watu walipomsifu tayari Sauli alimuonea wivu na kuanza uadui na Daudi, wako watu wanaweza kuanzisha uadui na wewe na wakakuchukia na kukupiga vita lakini sababu kubwa ni kuwa hawawezi kuvumilia Baraka zako!, angalia kuwa Sauli akimuwa mfalme na Daudi alikuwa mchunga kondoo tu, dunia ni yenye kushangaza kwa sababu wakati mwingine mtu mkubwa na mwenye nguvu kuliko wewe anakupiga vita wewe uliye mdogo kwa nini kwa sababu hawawezi kuvumilia Baraka zako!

 

4.       Wakati Mwingine tunapopandishwa Cheo.

 

Wako watu ambao wanaweza kushindwa kuvumilia Baraka zako kwa sababu eti wewe umekuwa mkubwa kuliko wao kwa sababu wewe una cheo kikubwa kuliko wao, unajua watu wanadhani cheo ni kuukata au kuuchinja au kuula, lakini Mungu huwa anatupa majukumu ili tuwatumikie watu hivyo kutokana na Baraka za kiungu Mungu anaweza kusababisha uinuliwe juu sana na ukawa na sifa njema lakini jambo la kushangaza ni kuwa wako watu hawataweza kustahimili kuinuliwa kwako na kwa sababu hiyo wataanza kupanga mikakati ya kibinadamu kabisa ili wakumalize kwa sababu hawawezi kuvumilia Baraka zako!

 

Daniel 6:1-5 “Ilimpendeza Dario kuweka juu ya ufalme maliwali mia na ishirini, wawe juu ya ufalme wote; na juu yao akaweka wakubwa watatu, na Danieli alikuwa mmoja wao; ili maliwali hawa watoe hesabu kwao, mfalme asipate hasara. Basi Danieli huyo alipata sifa kuliko wakubwa na maliwali, kwa kuwa roho bora ilikuwa ndani yake; naye mfalme akaazimu kumweka juu ya ufalme wote. Basi mawaziri na maamiri wakatafuta sana kupata sababu za kumshitaki Danieli kwa habari za mambo ya ufalme; lakini hawakuweza kuona sababu wala kosa; kwa maana alikuwa mwaminifu, wala halikuonekana kosa wala hatia ndani yake. Ndipo wale watu wakasema, Hatutapata sababu ya kumshitaki Danieli huyo, tusipoipata katika mambo ya sheria ya Mungu wake.”

 

Unaona watu wanapata taabu sana kwa sababu una cheo na unaupiga mwingi katika mamlaka uliyo nayo kwa hiyo zinatafutwa sababu ili wakukamate, uweze kutiwa hatiani, Daniel alianza kutafutia namna hii iko kila mahali, iwe ni makazini, au makanisani, na kwenye taasisi mbalimbali kuna watu ni waroho wa Madaraka wanatafuta kila linalowezekana wakuangushe tu na hawajisikii vizuri wewe ukitamalaki! Kwa nini  kwa sababu hawawezi kuvumilia Baraka zako!

 

5.       Wakati mwingine kwa sababu unajenga.

 

Wako watu wengine kwa sababu wewe uko kwenye ujenzi unajenga basi wivu unawainuka na wanatamani kupingana na kile unachikifanya, wakati nakumbuka nilipokuwa najenga nyumba yangu, wachwi walikuja na kufanya uchawi wao wa kusotea huu ni uchawi wa kuhakikisha kuwa nyumba inadumaa na haiwezi kujengeka kama unaishia kwenye linta inakuwa ni kwenye linta tu, lakini mimi nilimtegemea Mungu hata baada ya wachawi kusotea na kuacha kinyesi kwenye nyumba ile, nilimuomba Mungu na ujenzi ukaenda kwa kasi sana na nikafanikiwa na ndipo wachawi walipokuja waziwazi na kugombana na mimi kwa hasira kali sana kwa nini kwa sababu hawawezi kuvumilia Baraka zangu, Nehemia alipokuwa anaujenga ukuta wa Yerusalem maadui wa wayahudi walitoa maneno ya kufuru kwa sababu Nehemia na wayahudi walikuwa kwenye ujenzi ona

 

Nehemia 4:1-8 “Lakini ikawa, Sanbalati aliposikia ya kwamba tulikuwa tukiujenga ukuta, akaghadhibika, akaingiwa na uchungu sana, akawadhihaki Wayahudi. Akanena mbele ya nduguze na mbele ya jeshi la Samaria, akisema, Wayahudi hawa wanyonge wanafanyaje? Je! Watajifanyizia boma? Watatoa dhabihu? Au watamaliza katika siku moja? Je! Watayafufua mawe katika chungu hizi za kifusi, nayo yameteketezwa kwa moto? Basi Tobia, Mwamoni, alikuwa karibu naye, akasema, Hata hiki wanachokijenga, angepanda mbweha, angeubomoa ukuta wao wa mawe. Sikia, Ee Mungu wetu; maana tunadharauliwa; ukawarudishie mashutumu yao juu ya vichwa vyao, ukawatoe watekwe katika nchi ya uhamisho; wala usiusitiri uovu wao, wala isifutwe dhambi yao, mbele zako; kwa maana wamekukasirisha mbele ya hao wanaojenga. Basi tukaujenga ukuta; nao ukuta wote ukaungamanishwa kiasi cha nusu ya kimo chake; maana watu walikuwa na moyo wa kufanya kazi. Lakini ikawa, Sanbalati, na Tobia, na Waarabu, na Waamoni, na Waashdodi, waliposikia ya kuwa kazi ya kuzitengeneza kuta za Yerusalemu inaendelea, na ya kuwa mahali palipobomoka panaanza kuzibwa, basi wakaghadhibika mno; wakafanya shauri wote pamoja kuja kupigana na Yerusalemu, na kufanya machafuko humo.”

 

Unaona kuna watu wanaweza kutoa maneno ya kejeli kwako, au hata kughadhibika na kufanya machafuko lakini ukiangalia sababu kubwa ni kua hawawezi kuvumilia Baraka zako, wala usishangae, wala usifadhaike they can’t handle your blessing  wakati mwingine utajenga nyumba watasema ni nyumba basin i kakibanda tu ili mradi wakukatishe tama usiogope ni kwa sababu hawawezi kuvumilia Baraka zako!

 

6.       Wakati mwingine ili wakunyamazishe

 

Kuna watu wakati mwingine hawafurahii kuona ukivuma au ukisifiwa au jina lako likiwa na nguvu, au ukishangiliwa hivyo kutokana na wivu wanatamani wakunyamazishe, wanapoona unafanya vizuri unakubalika na una nafasi kubwa sana sifa zako zinaenea kila mahali utashangaa wanakunyamazisha au wanataka hata na watu wanaokusifia wanyamaze ona

 

Luka 19:37-40 “Hata alipokuwa amekaribia matelemko ya mlima wa Mizeituni, kundi zima la wanafunzi wake walianza kufurahi na kumsifu Mungu kwa sauti kuu, kwa ajili ya matendo yote ya uwezo waliyoyaona, wakasema, Ndiye mbarikiwa Mfalme ajaye kwa jina la Bwana; amani mbinguni, na utukufu huko juu. Baadhi ya Mafarisayo waliokuwa katika mkutano wakamwambia, Mwalimu, uwakanye wanafunzi wako. Akajibu, akasema, Nawaambia ninyi, wakinyamaza hawa, mawe yatapiga kelele.”

 

Unaona wakati mwingine unaweza kujikuta unanyamazishwa ziko namna nyingi watu watataka wakunyamazishe kwa sababu sifa zako zinaenea na kukua kwa kasi na wanajisikia vibaya hawawezi kustahimili, kwa nini hii ni kwa sababu hawawezi kuvumilia Baraka zako.!

 

7.       Wanataka uwasujudie

 

Kuna watu wengine huwa wakipata cheo tayari wanageuka kuwa miungu watu na wanataka uwatetemekee na kuwasujudia na ikiwa hutetemeki wala kuwasujudia wanachukia sana na hiyo inaweza kuwa sababu ya kuanzisha mapambanao na wewe, na hata kukuangamiza ona

 

Esta 5:9-13 “Basi Hamani alitoka siku ile kwa furaha na ukunjufu wa moyo; lakini Hamani alipomwona Mordekai mlangoni pa mfalme, ya kwamba hasimami wala kutetemeka mbele yake, alijaa ghadhabu juu ya Mordekai. Walakini Hamani akajizuia, akaenda zake nyumbani kwake; akatuma kuwaita rafiki zake na Zereshi mkewe. Naye Hamani akawasimulia habari za fahari ya mali zake, na wingi wa watoto wake, nayo mambo yote pia ambayo mfalme amemfanikisha katika hayo, na jinsi alivyompandisha juu ya maakida na watumishi wa mfalme. Zaidi ya hayo Hamani akasema, Naye malkia Esta hakumkaribisha mtu ye yote pamoja na mfalme katika karamu aliyoiandaa, ila mimi peke yangu; hata na kesho pia nimealikwa naye pamoja na mfalme. Bali haya yote yanifaa nini, pindi nimwonapo yule Mordekai, Myahudi, ameketi mlangoni pa mfalme?

 

unaona ni kwanini Hamani pamoja na fahari yake aliyokuwa nayo alikuwa hajisikii raha ? kwa sababu alikuwa anataka asujudiwe, wako watu wanataka watetemekewe, wababaikiwe kwa sababu tu eti wana madaraka makubwa wa kutetemekewa ni Mungu tu yeye ndiye mwenye destiny Hatima ya maisha yetu, na sio mwanadamu

 

Esta 3:1-6 “Baada ya hayo mfalme Ahasuero alimwongezea cheo Hamani bin Hamedatha, Mwagagi, akampandisha, akamwekea kiti chake juu ya maakida wote waliokuwapo pamoja naye. Nao watumishi wote wa mfalme, walioketi mlangoni pa mfalme, wakainama na kumsujudia Hamani, maana ndivyo alivyoamuru mfalme kwa habari zake. Bali Mordekai hakuinama, wala kumsujudia. Basi watumishi wa mfalme walioketi mlangoni pa mfalme wakamwambia Mordekai, Mbona wewe waihalifu amri ya mfalme? Ikawa, waliposema naye kila siku asiwasikilize, wakamwarifu Hamani, ili kuona kama mambo yake Mordekai yatasimama; maana alikuwa amewaambia ya kuwa yeye ni Myahudi. Hata Hamani alipoona ya kwamba Mordekai hainami wala kumsujudia, alighadhibika sana. Akaona si shani kumtia mikono Mordekai peke yake; maana wamemjulisha kabila yake Mordekai; kwa hiyo Hamani alitaka kuwaangamiza Wayahudi wote waliokuwa wakikaa katika ufalme wote mzima wa Ahasuero, yaani, watu wake Mordekai.”

 

Umeona wako watu wanadhani wewe huwaheshimu kwa sababu huwasujudii sie wengine ni wayahudi tunaheshimu kila mtu lakini hatuabudu watu, tunamwabudu Mungu peke yake kama maandiko yalivyotuelekeza Luka 4:8 “Yesu akajibu akamwambia, Imeandikwa, Msujudie Bwana Mungu wako, umwabudu yeye peke yake  wakati mwingine visa na mikasa huinuka kwa sababu watu wanataka kuabudiwa, mtu unamuheshimu laki ni anataka kuvuka mipaka ya kiheshima na kwenda mbali zaidi, Mordekai aliyekuwa myahudi alikuwa amejifunza kuwa mwanadamu wa kawaida muheshimu lakini wakumuinamia  na kumtetemekea ni Mungu peke yake anayestahili kuabudiwa na kusujudiwa wengine wakiona hufanyi hivyo hawawezi kuvumilia kwa sababu hauabudu mwanadamu.!

 

8.       Wakati mwingine kwa sababu unatumiwa na Mungu kuliko wao

 

Kuna watu wakati mwingine hawafurahii kuona namna Mungu anavyokutumia katika karama na vipawa mbalimbali kuliko wao na kwa sababu hiyo watajisikia wivu moyoni na wakati mwingine watazusha maneno ya uwongo kwa kusudi la kukuchafulia huduma yako, wanaweza kusema unafanya mioujiza kwa kutumia nguvu za giza, wanaweza kusema wewe ni freemason, wanaweza kusema wewe ni mchawi, anaweza kusema wewe ni imani potofu, hutumii jina la Yesu na kadhalika hiii yota inafanyika kwa sababu hawawezi kuvumilia Baraka na upako ambao Mungu ameweka ndani yako ona

 

Mathayo 12:22-24 “Wakati ule akaletewa mtu mwenye pepo, kipofu, naye ni bubu; akamponya, hata yule bubu akanena na kuona. Makutano wote wakashangaa, wakasema, Huyu siye mwana wa Daudi? Lakini Mafarisayo waliposikia, walisema, Huyu hatoi pepo, ila kwa Beelzebuli mkuu wa pepo

 

Unaona Mafarisayo hawakufurahia Yesu kukubalika kutokana na ishara na miujiza aliyokuwa akiifanya, sisis nasi Yesu alituambia kuwa Mwanafunzi hawezi kumpita Mwalimu wake maana yake yale majaribu ambayo Mwalimu aliyapitia sisi nasi tutayapitia na kuzidi, tumetumwa kama Kondoo katikati ya mbwa mwitu, lazima adui wa Baraka za kiungu ndani yetu watajitokeza na kuleta kila aina ya upinzani katika jambo lolote ambalo kwalo Mungu ameweka mkono wake usiogope jambo kubwa na la msingi la kukumbuika ni kuwa hawawezi kuvumilia Baraka zako!

Tumeona katika Mstari wetu wa Msingi kuhusu baba yetu wa Imani nabii Isaka ya kuwa Mungu alimbariki upeo, ilikuwa kuna njaa katika nchi ya kanaani na ilikuwa ni kawaida kuwa kukiwa na njaa kama ilivyokuwa wakati wa Ibrahimu baba yake, wao walikimbilia Misri kwa sababu ya chakula, hata hivyo Mungu alimuonya Isaka kuwa asishuke kwenda Misri, na Mungu akaweka Baraka zake, Isaka na baba yake Ibrahimu walikuwa ni wataalamu wa kuchimba visima, walifahamu namna na jinsi ya kuchimba maji, na huenda pia Isaka alikuwa na ujuzi wa kumwagilia, njaa ilipokuwa kali yeye alipanda mbegu na bila shaka alimwagilia hivyo Mungu alimbariki na akampa kuvuna mara mia lakini sio hivyo tu mali yake iliongezeka na umaarufu wake ukawa mkubwa mno, hivyo akastawi na kuwa mtu mkubwa sana, wafilisti walianza kuona wivu, kila kisima alichokichimba wao walikigombea na kukifukia au kudai kuwa ni cha kwao, Biblia imeweka wazi kuwa wafilisti WAKAMHUSUDU yaani maana yake waluiona wivu tena wivu wenye uchungu, Isaka alikuwa mpenda amani hivyo aliwaachia na kuchimba kingine lakini walifanya fitina hii ama ile na mwisho wakaona haya Isaka akachimba na kingine na wakapata Maji na wakakiita kisima kile REHOBOTHI maana yake sasa Bwana ametufanyia nafasi, Isaka aliteseka kwa sababu ya Baraka zake, yako mateso mengine unayapitia na changamoto nyingine unazipitia sio kwa sababu umemkosea Mungu bali kwa sababu Mkono wa Mungu uko juu yako na wanaokuzunguka hawawezi kustahimili wala kuvumilia aina ya upako ulio nao, aina ya huduma uliyo nayo aina ya Baraka ulizoanazo, aina ya uimbaji unaoimba, aina ya mavazi unayovaa, aina ya uzuri ulio nao na kila aina ya Baraka kwa kawaida ina tabia ya kuvutia watu na maadui kwa nini ulipobarikiwa wengine walikukimbia ni kwa sababu hawawezi kuvumilia Baraka zako!, wako ambao hawatavumilia wewe kuzaa, hawatavumilia wewe kuolewa, hawatavumilia we kuwa na mtoto, hatawatavumilia wewe kufanikiwa au kua na ustawi wa aina yoyote ilekatika jamii kwa nini kwa sababu wako watu watakupoenda na kukusoegelea lakini wako wengine hawataweza kuvumilia Baraka zako! Bwana Mungu wa Baba zangu Ibrahim, Isaka na Yakobo na akufanyie nafasi, ili ufurahie Baraka zako bila usumbufu kutoka kwa maadui katika jina la Yesu nakuombea amen!

 

Na Rev. Innocent Kamote

Mkuu wa wajenzi mwenye Hekima!

Jumapili, 8 Mei 2022

Mfalme juu ya Punda


Mathayo 21:1-5Hata walipokaribia Yerusalemu, na kufika Bethfage, katika mlima wa Mizeituni, ndipo Yesu alipotuma wanafunzi wawili akiwaambia, Enendeni mpaka kijiji kile kinachowakabili, na mara mtaona punda amefungwa, na mwana-punda pamoja naye; wafungueni mniletee. Na kama mtu akiwaambia neno, semeni, Bwana anawahitaji; na mara huyo atawapeleka. Haya yote yamekuwa, ili litimie neno lililonenwa na nabii, akisema, Mwambieni binti Sayuni Tazama, mfalme wako anakuja kwako, Mpole, naye amepanda punda, Na mwana-punda, mtoto wa punda.”


Utangulizi:

Ni muhimu kufahamu kwamba tukio la Yesu Kristo kupokelewa kwa shangwe jijini Yerusalem, lilikuwa ni tukio la kipekee sana lililofanywa na watu, sawa kabisa na namna watu wanavyompokea mfalme, tukio hili halikuwa tukio la bahati mbaya kwani vilevile lilikuwa ni sehemu ya kutimizwa kwa maandiko ya kinabii kuhusu kuja kwa mfalme wa kipekee ambaye angejibu mahitaji yote ya wanadamu Nabii Zekaria alilitabiri tukio hili miaka 400 kabla ya kuzaliwa kwa Yesu ona;-

Zecharia 9:9Furahi sana, Ee binti Sayuni; Piga kelele, Ee binti Yerusalemu; Tazama, mfalme wako anakuja kwako; Ni mwenye haki, naye ana wokovu; Ni mnyenyekevu, amepanda punda, Naam, mwana-punda, mtoto wa punda.”

Swali moja kubwa ambalo wanafunzi wengi wa maandiko hupenda kujiuliza ni kwamba, iko wazi kuwa Yesu alipokelewa Yerusalem kwa shangwe kubwa sana watu walimfurahia kwa matawi ya mitende na hata kutandaza nguo zao njiani, lilikuwa ni tukio la kipekee sana ambalo hakuna mfalme amewahi kufanyiwa,Mungu roho Mtakatifu aliinua mioyo ya watu na wakasangilia kwa nguvu sana kuingia kwa Maishi pale Sayuni, lakini swali kubwa kwanini mfalme huyu awe amepanda punda?  Hili ndio swali kubwa na la Muhimu kwa kila mmoja wetu kujiuliza na kutafuta majibu.

Wafalme huja na Majibu ya mahitaji ya watu!

Moja ya Kazi kubwa sana ya wafalme wa zamani na labda huenda hata sasa ilikuwa ni pamoja na kutawala mfalme alipaswa kuwa na majibu ya aina yoyote dhidi ya mahitaji ya watu wake, wafalme walitakiwa kutatua changamoto zilizowakabili watu hata kuamua kesi za aina mbalimbali mfano;- 

1Wafalme 3:16-28 “Ndipo wanawake wawili, makahaba, walimwendea mfalme, wakasimama mbele yake. Na mwanamke mmoja akasema, Ee bwana wangu, mimi na mwanamke huyu tunakaa katika nyumba moja; nami nalizaa nilipokuwa pamoja naye nyumbani. Kisha, siku ya tatu baada ya kuzaa kwangu, ikawa mwanamke huyu naye akazaa; na sisi tulikuwa pamoja; hapakuwa na mtu mwingine pamoja nasi nyumbani, isipokuwa sisi wawili tu. Na mtoto wa mwanamke huyu akafa usiku, maana alimlalia. Akaondoka kati ya usiku, akamwondoa mtoto wangu ubavuni pangu, mimi mjakazi wako nilipokuwa usingizini, akamweka kifuani pake, na mtoto wake mwenyewe, aliyekuwa amekufa, akamweka kifuani pangu. Nilipoondoka asubuhi nimnyonyeshe mtoto wangu, kumbe? Amekufa. Hata asubuhi nilipomtazama sana, kumbe! Siye mtoto wangu niliyemzaa. Ndipo yule mwanamke wa pili akasema, Sivyo hivyo; bali mtoto wangu ndiye aliye hai, na mtoto wako ndiye aliyekufa. Na mwenzake akasema, Sivyo hivyo; bali mtoto wako ndiye aliyekufa, na mtoto wangu ndiye aliye hai. Ndivyo walivyosema mbele ya mfalme.  Ndipo mfalme akasema, Huyu anasema, Mtoto wangu yu hai, na mtoto wako amekufa. Na huyu anasema, Sivyo hivyo; bali mtoto aliyekufa ni wako, na mtoto aliye hai ni wangu. Mfalme akasema, Nileteeni upanga. Wakaleta upanga mbele ya mfalme. Mfalme akasema, Mkate mtoto aliye hai vipande viwili, kampe huyu nusu, na huyu nusu. Ndipo mwanamke yule, ambaye mtoto aliye hai ni wake, akamwambia mfalme kwa maana moyoni mwake alimwonea mtoto wake huruma, akasema, Ee bwana wangu, mpe huyu mtoto aliye hai, wala usimwue kamwe. Lakini yule mwingine akasema, Asiwe wangu wala wako; na akatwe. Ndipo mfalme akajibu, akasema, Mpe huyu wa kwanza mtoto aliye hai, maana yeye ndiye mama yake. Na Israeli wote wakapata habari za hukumu ile aliyoihukumu mfalme wakamwogopa mfalme; maana waliona ya kuwa hekima ya Mungu ilikuwa ndani yake, ili afanye hukumu.”

Wafalme walitakiwa kujibu hoja zozote ngumu za watu wao waliowatembelea kuhitaji msaada katika maeneo mbalimbali ya maisha yao 1Wafalme 10:1 “Na malkia wa Sheba aliposikia habari za Sulemani juu ya jina la Bwana, alikuja ili amjaribu kwa maswali ya fumbo.” Biblia ya kiingereza inatumia maneno “she came to test her with HARD questions       Hata hivyo Mfalme Suleimani pia aliweza kutoa majibu ya maswali yote aliyouliza malikia wa Sheba. Hata hivyo maandiko pia yanatueleza kuwa kuna wakati ambapo wafalme walikosa majibu na uwezo wa kutatua changamoto kadhaa na hivyo walilia, na kufunga na kuvaa magunia au kurarua mavazi yao. Angalia kwa mfano:-

2Wafalme 6:25-30 “Njaa ikawa kuu huko Samaria; na tazama, wakauhusuru, hata kichwa cha punda kikapata kuuzwa kwa vipande themanini vya fedha, na kibaba cha mavi ya njiwa kwa vipande vitano vya fedha. Ikawa mfalme wa Israeli alipokuwa akipita ukutani, mwanamke mmoja akamwita akisema, Unisaidie, bwana wangu, mfalme. Akasema, Bwana asipokusaidia, nikusaidieje mimi? Ya sakafuni, au ya shinikizoni? Mfalme akamwambia, Una nini? Akajibu, Mwanamke huyu aliniambia, Mtoe mtoto wako, tumle leo, na mtoto wangu tutamla kesho. Basi, tukamtokosa mtoto wangu, tukamla; nikamwambia siku ya pili, Mtoe mtoto wako, tumle; naye amemficha mtoto wake. Ikawa, mfalme alipoyasikia maneno ya huyo mwanamke, aliyararua mavazi yake; (naye alikuwa akipita juu ya ukuta;) na watu wakaona, na tazama, alikuwa amevaa magunia ndani mwilini mwake.”

Unaona kwa msingi huo Mfalme alikuwa na kazi ngumu ya kutatua changamoto za maisha ya watu,  ukiacha swala la kutatua changamoto ya maisha ya watu, mfalme pia alitakiwa kuwa mtu wa vita na mwenye uwezo wa kutwatetea watu wake dhidi ya adui zao kwa kupigana kwa silaha na kwa uwezo wa kujihami, wafalme walipaswa kuwa watu wa vita, Heshima ya mfalme ilikuwa kupitia uwezo wake wa kuamua mambo na kuwapigania watu wakena kuwashindia dhidi ya adui zao, mfano

 1Samuel 17:1- 11. Wakati huo Wafilisti walikusanya majeshi yao kwa vita, nao wakakusanyika huko Soko, ulio mji wa Yuda, wakatua kati ya Soko na Azeka, katika Efes-damimu. Naye Sauli na watu wa Israeli wakakusanyika, wakatua katika bonde la Ela, nao wakapanga vita juu ya hao Wafilisti. Wafilisti wakasimama juu ya mlima upande huu, na Waisraeli wakasimama juu ya mlima upande huu, napo palikuwa na hilo bonde katikati. Ndipo akatoka shujaa katika kambi ya Wafilisti, aliyeitwa Goliathi, wa Gathi, ambaye urefu wake ulikuwa mikono sita na shibiri moja. Alikuwa na chapeo ya shaba kichwani, tena amevaa darii ya shaba; na uzani wake ile darii ya shaba ulikuwa shekeli elfu tano za shaba. Tena amevaa mabamba ya shaba miguuni mwake, naye alikuwa na mkuki wa shaba kati ya mabega; yake. Na mti wa fumo lake ulikuwa kama mti wa mfumaji; na kichwa cha mkuki wake kilikuwa shekeli mia sita za chuma uzito wake; na mtu aliyemchukulia ngao yake akamtangulia. Naye akasimama, akawapigia kelele majeshi ya Israeli akawaambia, Mbona mmetoka kupanga vita? Je! Mimi si Mfilisti, na ninyi si watumishi wa Sauli? Jichagulieni mtu, akanishukie mimi. Kama akiweza kupigana nami na kuniua, sisi tutakuwa watumwa wenu; nami nikimshinda yeye na kumwua, ninyi mtakuwa watumwa wetu, na kututumikia. Yule Mfilisti akasema, Nayatukana leo majeshi ya Israeli; nipeni mtu tupigane. Basi Sauli na Israeli wote waliposikia maneno hayo ya Mfilisti, wakafadhaika na kuogopa sana.”

Mfalme juu ya Punda !

Sasa moja ya tukio la kushangaza ni kuwa pamoja na kuwa wafalme walikuwa ni watu waliotakiwa kujibu hoja na mahitaji ya watu ya aimna mbalimbali na kuwashindia watu vita dhidi ya adui zao, ni muhimu kufahamu kuwa wafalme walipotaka kuonyesha nguvu zao na ukuu wao wakati wote walitumia farasi katika kusafiri kwao, Farasi ilikuwa ni alama ya vita na ufahari na utajiri, kwa hiyo kila mfalme aliyekuwa anataka kuonyesha ufahari wake alitumia farasi, farasi ni mnyama anayeonyesha uhodari, wakati punda ni mnyama anayeonyesha huduma,  kama watu walikuwa wakijivuna walijivunia magari yao ya farasi kwani hayo ndio yalikuwa yakidhihirisha nguvu na uwezo wao

Zaburi 20:1-9 “Bwana akujibu siku ya dhiki, Jina la Mungu wa Yakobo likuinue. Akupelekee msaada toka patakatifu pake, Na kukutegemeza toka Sayuni. Azikumbuke sadaka zako zote, Na kuzitakabali dhabihu zako. Akujalie kwa kadiri ya haja ya moyo wako, Na kuyatimiza mashauri yako yote. Na tuushangilie wokovu wako, Kwa jina la Mungu wetu tuzitweke bendera zetu. Bwana akutimizie matakwa yako yote. Sasa najua kuwa Bwana amwokoa masihi wake;Atamjibu kutoka mbingu zake takatifu.Hawa wanataja magari na hawa farasi, Bali sisi tutalitaja jina la Bwana, Mungu wetu. Wao wameinama na kuanguka, Bali sisi tumeinuka na kusimama. Bwana, umwokoe mfalme, Utuitikie siku tuitayo.”

Watu wanachohitaji ni kuokolewa kutoka katika changamoto zinazowakabili, haijalishi mfalme anakuja namna gani, anaweza akaja na magari ya farasi lakini akawa hana majibu ya kutosheleza mioyo ya watu wake Zekaria alitabiri kuwa anakuja mfalme mnyenyekevu, mpole hana majivuno wala majigambo wala hana nia ya kutafuta kiki au ufahari yeye anakuja na wokovu anakuja na kifurushi kitakachotuletea amani ni mfalme wa tofauti mwenye uwezo wa kutatua changamoto za watu kwa kiwango kikubwa sana yeye anatabiriwa kuwa angekuja akiwa amepanda punda na mwana punda mtoto wa punda, hii ilikuwa ni ishara madhubuti ya kumtambua mfalme huyo mwenye nguvu zote lakini mnyenyekevu!

 Zakaria 9:9-10 “Furahi sana, Ee binti Sayuni; Piga kelele, Ee binti Yerusalemu; Tazama, mfalme wako anakuja kwako; Ni mwenye haki, naye ana wokovu; Ni mnyenyekevu, amepanda punda, Naam, mwana-punda, mtoto wa punda. Na gari la vita nitaliondoa liwe mbali na Efraimu, na farasi awe mbali na Yerusalemu, na upinde wa vita utaondolewa mbali; naye atawahubiri mataifa yote habari za amani; na mamlaka yake yatakuwa toka bahari hata bahari, na toka Mto hata miisho ya dunia.”

Maandiko yanaonyesha kuwa mfalme huyu

o   Atakomesha vita

o   Silaha za vita kama upinde utaondolewa mbali

o   Hatakuja na majeshi

Yeye atatangaza amani kwa mataifa yote na ufalme wake utakuwa ni wa dunia nzima, Luka 2:14 “Atukuzwe Mungu juu mbinguni, Na duniani iwe amani kwa watu aliowaridhia.” Mfalme atakayeingia Yerusalem, yaani katika mlima wa Sayuni akiwa juu ya Punda, ni simple but powerful ni mnenyekevu na mpole lakini ana majibu yote yeye atatoa suluhu ya mahitaji yetu yote na hivyo tunachopaswa kusema ni Hosana mwana wa Daudi, mfalme mwenye majibu ya wokovu wako haji na vifaru, haji na ufahari wowote anakuja na mwana punda, humble but very powerful, huyu ndiye mfalme aliyetabiriwa na Zekaria na Mathayo anatudhihirishia kuwa Yesu ndiye mfalme huyu ambaye amekuja kulitimiza andiko, ana hekima kuliko suleimani na ana nguvu kuliko Daudi, yeye atatupigania na hakuna kinachoweza kusimama mbele yake yeye ndiye mtetezi wa adui zetu na mkombozi wetu dhidi ya unyonge si mwingine ni Yesu !

Rev. Innocent Kamote

Mkuu wa wajenzi Mwenye Hekima!

Jumatatu, 2 Mei 2022

Shika sana ulichonacho!


Ufunuo 3:10-12 “Kwa kuwa umelishika neno la subira yangu, mimi nami nitakulinda, utoke katika saa ya kuharibiwa iliyo tayari kuujilia ulimwengu wote, kuwajaribu wakaao juu ya nchi. Naja upesi. Shika sana ulicho nacho, asije mtu akaitwaa taji yako. Yeye ashindaye, nitamfanya kuwa nguzo katika hekalu la Mungu wangu, wala hatatoka humo tena kabisa, nami nitaandika juu yake jina la Mungu wangu, na jina la mji wa Mungu wangu, huo Yerusalemu mpya, ushukao kutoka mbinguni kwa Mungu wangu, na jina langu mwenyewe, lile jipya.”


Utangulizi:

Wito unatolewa kwa kanisa na kila mwanadamu mmoja mmoja kushika sana au kwa lugha nyingine kutunza sana kile alichonacho, asije mtu akaitwaa taji yako, Hii ni kwa sababu kuja kwa Yesu kunakaribia, lakini sio hivyo tu kuna misukumo mingi sana duniani na nguvu kubwa ya upinzani ambayo iko kinyume na kile ambacho Mungu amekubarikia kwacho katika maisha haya, Yesu Kristo alikuwa akizungumza na kutoa ujumbe wake kwa makanisa saba yaliyokuwepo katika Asia ndogo huko uturuki, akiyaonya na kuwatia moyo katika maswala mbalimbali na hapa anazungumza na kanisa la Filadelfia ambalo kimsingi lilikuwa na mambo mazuri ukilinganisha na mengine na Yesu anawataka wajitunze, wawe makini ili wasije wakapoteza kile walicho nacho ambacho ni kizuri, kimsingi sina mpango wa kuzungumzia Makanisa yale saba,wala nyakati zile saba za historia ya kanisa kwani vyote vinaweza kutumika kuzungumza na kanisa, lakini Mpango wangu ni kuzungumza na wewe au na hata mimi mwenyewe, ya kwamba mara kadhaa Mungu ametubariki kwa mambo mengi mazuri, mfano, Kazi nzuri, Ndoa nzuri, kibali, mambo mema, vipawa, kujulikana, na kadhalika ziko zawadi nyingi na nafasi nyingi nzuri ambazo Mungu ametubarikia nazo katika maisha yetu lakini wengi wetu huwa tunajikuta nafasi zile, vipawa vile, zawadi zile na Baraka zile hatuna uwezo wa kuzitunza, au tunazipoteza kabisa hii ni kwa sababu shetani anavutiwa sana na kila jambo jema ambalo Mungu amewekeza katika maisha yetu na hivyo anakusudia kutuharibia, wakati mwingine tunapambana kufa na kupona na kumwaga jasho letu jingi kwaajili ya jambo Fulani lakini unapokuja wakati wa mavuno adui anakuja na kutuharibia na kuvuruga kabisa mpango wa Mungu katika maisha yetu, hapa ndipo mahali Yesu anatutaka tushike sana kile tulichonacho!  Hali mkama hii iliwasumbua sana Israel wakati wa waamuzi kabla Gideoni hajaitwa ona!;- 

Waamuzi 6:2-6,11 “Mkono wa Midiani ulikuwa na nguvu juu ya Israeli; tena kwa sababu ya Midiani wana wa Israeli walijifanyia hayo mashimo yaliyo milimani, na hayo mapango, na hizo ngome. Basi ikawa, hapo Israeli walipokuwa wamepanda mashamba, Wamidiani wakakwea, na Waamaleki, na hao wana wa mashariki; wakakwea juu yao; wakapanga marago juu yao, na kuyaharibu hayo maongeo ya nchi, hata ufikapo Gaza, wala hawakuacha katika Israeli riziki ziwazo zote; kondoo, wala ng'ombe, wala punda. Kwa maana walikwea na ng'ombe zao na hema zao, wakaja mfano wa nzige kwa wingi; wao na ngamia zao pia walikuwa hawana hesabu; nao waliingia katika hiyo nchi ili kuiharibu. Israeli walitwezwa sana kwa sababu ya Wamidiani; nao wana wa Israeli wakamlilia Bwana. Malaika wa Bwana akaenda akaketi chini ya mwaloni uliokuwa katika Ofra, uliokuwa mali yake Yoashi, Mwabiezeri; na mwanawe Gideoni alikuwa akipepeta ngano ndani ya shinikizo, ili kuificha machoni pa Wamidiani.”

Unaona shetani atasubiri umetaabika sana na pale unapokuwa unatarajia kuwa utapumzika utagundua kuwa ndio kwanza vita inaanza upya na ni kama hakuna kulala na endapo utajisahau shetani atachukua mateka kila kitu na kukuacha ukiwa unalia na kulalamika wakati kilikuwa mikononi mwako na kiko kwenye uwezo wako!

o   Maana ya neno taji

o   Shika sana kile ulichonacho!

Maana ya neno taji:

Neno taji katika lugha ya kiyunani linasomeka kama neno “STEMMA” kwa kiibrania ni “TIARA” ambayo maana yake ni kwa kiingereza “Top”, au “Climax”, au “The highest” au “Uppermost point” au “surface of something”, au “Exeed”  kwa hivyo neno taji maana yake ni kilele cha ubora, ni ile hali ya kuwa juu, kama ni nyota kuwa na mwangaza mkubwa zaidi kuliko wengine, au hali ya kuwa na kitu cha ziada kinachozidi wengine, ni kilele cha furaha yako, kwa hiyo neno la Mungu linatuonya kutunza kile kilichobora ambacho Mungu ametupa kwa sababu adui yetu shetani hawezi kufurahia kile ulicho nacho au kile ambacho ndio shauku yako uweze kukifikia, Mungu anatutaka kutokudharau na kufikiri kuwa kile tulichonacho sio bora wakati kuna watu wanatamani ukipoteze ili wakipate, kwa msingi huo ni muhimu kufahamu kuwa tunapokuwa duniani tuko kwenye uwanja wa vita ambapo kuna mapambano ambapo, kile ulichonacho ambacho wewe unaweza kuwa huujali na wala haumshukuru Mungu ya kuwa unacho kuna wengine wanakitamani na watapigana wakipate kwa msingi huo lazima ujue namna ya kukitunza taji yako inaweza kuchukuliwa na akapewa mtu mwingine ona:-

2Samuel 12:29-31 “Basi Daudi akawakusanya watu wote akaenda Raba, akapigana nao, akautwaa. Kisha akamnyang'anya mfalme wao taji toka kichwani pake; na uzani wake ulikuwa talanta ya dhahabu, nayo ilikuwa na vito vya thamani ndani yake; akavikwa Daudi kichwani. Akazitoa nyara za huo mji, nyingi sana. Naye akawatoa watu waliokuwamo, akawaweka kwenye kazi ya misumeno, na sululu za chuma, na mashoka ya chuma, akawatumikisha, tanuuni mwa matofali ndivyo alivyoifanya miji yote ya wana wa Amoni. Kisha Daudi akarudi na watu wote Yerusalemu.”

Ni muhimu kukumbuka kuwa kile unachokitamani wewe kuna na wenzako wanakitamani na kama utakuwa dhaifu kuna watu watapita mbele yako na watakichukua, usifikiri kuwa kuna mtu atakubeba au kukuhurumia, hakuna wa kukubeba lazima wewe mwenyewe upambane, Mungu anaweza kuachilia Baraka Fulani, lakini ni jukumu letu sisi kulinda, ukitegemea wanadamu wakubebe kumbuka nao wana mahitaji yao watakuacha utasota sana watapita mbele yako na watachukua kile wewe unatamani kuwa nacho na kukuacha unalalamika tu

Yohana 5:2-7 “Na huko Yerusalemu penye mlango wa kondoo pana birika, iitwayo kwa Kiebrania Bethzatha, nayo ina matao matano. Ndani ya hayo jamii kubwa ya wagonjwa walikuwa wamelala, vipofu, viwete, nao waliopooza, [wakingoja maji yachemke. Kwa maana kuna wakati ambapo malaika hushuka, akaingia katika ile birika, akayatibua maji. Basi yeye aliyeingia wa kwanza baada ya maji kutibuliwa, akapona ugonjwa wote uliokuwa umempata.] Na hapa palikuwa na mtu, ambaye amekuwa hawezi muda wa miaka thelathini na minane. Yesu alipomwona huyu amelala, naye akijua ya kuwa amekuwa hali hiyo siku nyingi, alimwambia, Wataka kuwa mzima? Yule mgonjwa akamjibu, Bwana, mimi sina mtu wa kunitia birikani, maji yanapotibuliwa; ila wakati ninapokuja mimi, mtu mwingine hushuka mbele yangu.”

Wakati wote unaweza kuona kama kuna kitu unakitamani ni lazima uchukue hatua wewe mwenyewe na usisubiri mwanadamu aje akusaidie, lazima upambane kuhakikisha kuwa unafikia kilelelcha furaha yako au hakikisha kuwa unamuita Yesu na kumuomba akusaidie haja ya moyo wako!.

Mungu anapokuwa amekubariki kwa kitu Fulani adui wakati wote anavutiwa na kitu hicho, na atainuka kupigana na kitu ambacho Mungu anataka au amekufanyia, wakati wote adui  atakuja wakati mambo yanapokaribia kuwa mazuri, baada ya wewe kutaabika sana ndipo anapokuja kuteka na kumbuka wakati wote utakuwa mwenyewe ukipambana ukifanikiwa watu wengi sana watakuzunguka, ukifeli kila mmoja atakukimbia, watu hawatakushambulia kwa sababu uko kama wao watakushambulia kwa sababu una taji, una kitu cha ziada umewazidi, una mambo mazuri, una nyumba nzuri, una gari nzuri, una cheo kizuri, una mshahara mzuri, una mafanikio, una kibali, una mvuto, una mke mzuri, una mume mzuri, una kipato kizuri, unazalisha mazao, unafanya vizuri, au hata una umbo zuri, kaa duniani na usifanye lolote lile uone kama kuna atakayepambana na wewe, watu watakushambulia kwa sababu una mafanikio na Mungu ameweka mkono wake kwako kwa hiyo utapigwa vita ili uwaondokee hawataki uwe una ushuhuda wa Baraka za Mungu kwako!

Daniel 6:1-4 “Ilimpendeza Dario kuweka juu ya ufalme maliwali mia na ishirini, wawe juu ya ufalme wote; na juu yao akaweka wakubwa watatu, na Danieli alikuwa mmoja wao; ili maliwali hawa watoe hesabu kwao, mfalme asipate hasara. Basi Danieli huyo alipata sifa kuliko wakubwa na maliwali, kwa kuwa roho bora ilikuwa ndani yake; naye mfalme akaazimu kumweka juu ya ufalme wote. Basi mawaziri na maamiri wakatafuta sana kupata sababu za kumshitaki Danieli kwa habari za mambo ya ufalme; lakini hawakuweza kuona sababu wala kosa; kwa maana alikuwa mwaminifu, wala halikuonekana kosa wala hatia ndani yake.”     

Unaona wakati wote unapokuwa na kitu cha ziada wewe ndio utakuwa unatafutwa, ili ushuhuda wa Mungu kuwa amekutendea mema uweze kupotea kwa sababu wengine watasikia na kumtukuza Mungu kwa yale ambayo Mungu amekufanyia sasa adui akufurahie kwa sababu gani? Shetani akufurahie wewe kwa lipi?

Shika sana ulichonacho!

Ni jukumu lako kuhakikisha kuwa wakati wote unapambana kulinda kile ambacho Mungu amekubariki kwacho, Baraka za Mungu katika maisha yetu zinavutia maadui hivyo wakati wote lazima ujifunze kujihami na kujilinda Yesu aliliambia kanisa la Filadelfia kuwa kwa kuwa umeishika sana subira yangu nani nitakulinda, ziko kanuni ambazo kwazo zinauwezo wa kutulinda

1.       Lazima tutumaini Mungu na kumtegemea yeye Zaburi ya 91:1-9 “Aketiye mahali pa siri pake Aliye juu Atakaa katika uvuli wake Mwenyezi. Nitasema, Bwana ndiye kimbilio langu na ngome yangu, Mungu wangu nitakayemtumaini. Maana Yeye atakuokoa na mtego wa mwindaji, Na katika tauni iharibuyo. Kwa manyoya yake atakufunika, Chini ya mbawa zake utapata kimbilio; Uaminifu wake ni ngao na kigao. Hutaogopa hofu ya usiku, Wala mshale urukao mchana, Wala tauni ipitayo gizani, Wala uele uharibuo adhuhuri, Ijapo watu elfu waanguka ubavuni pako. Naam, kumi elfu mkono wako wa kuume! Hata hivyo hautakukaribia wewe. Ila kwa macho yako utatazama, Na kuyaona malipo ya wasio haki.  Kwa kuwa Wewe Bwana ndiwe kimbilio langu; Umemfanya Aliye juu kuwa makao yako.”

 

2.       Uwe mwaminifu Daniel 6:16-22 “Basi mfalme akatoa amri, nao wakamleta Danieli, wakamtupa katika tundu la simba. Mfalme akanena, akamwambia Danieli, Mungu wako unayemtumikia daima, yeye atakuponya. Likaletwa jiwe, likawekwa mdomoni mwa lile tundu; naye mfalme akalitia muhuri kwa muhuri yake mwenyewe, na kwa muhuri ya wakuu wake, lisibadilike neno lo lote katika habari za Danieli. Kisha mfalme akaenda nyumbani kwake, akakesha usiku kucha, akafunga; na vinanda havikuletwa mbele yake; na usingizi wake ukampaa. Asubuhi mfalme akaondoka mapema, akaenda kwa haraka mpaka penye lile tundu la simba. Naye alipolikaribia lile tundu, akamlilia Danieli kwa sauti ya huzuni; mfalme akanena; akamwambia Danieli, Ee Danieli, mtumishi wa Mungu aliye hai, je! Mungu wako, unayemtumikia daima, aweza kukuponya na simba hawa? Ndipo Danieli akamwambia mfalme, Ee mfalme, uishi milele. Mungu wangu amemtuma malaika wake, naye ameyafumba makanwa ya simba, nao hawakunidhuru; kwa kuwa mbele zake mimi nalionekana kuwa sina hatia; tena, mbele yako, Ee mfalme, sikukosa neno.”            

 

3.       Usikubali kupeleka ibada kwa mwanadamu, maandko yako wazi kuwa amelaaniwa mtu yule amtegemeaye mwanadamu na kumfanya mwanadamu kuwa kinga yake, wokovu wa kweli kwetu hautoki kwa mwanadamu mtumaini Mungu na kumtegemea yeye tu naye atakusaidia

 

Daniel 3:12-27 “Wako Wayahudi kadha wa kadha uliowaweka juu ya mambo ya wilaya ya Babeli, yaani, Shadraka, na Meshaki, na Abednego; watu hawa, Ee mfalme, hawakukujali wewe; hawaitumikii miungu yako, wala kuiabudu ile sanamu ya dhahabu uliyoisimamisha. Basi Nebukadreza akatoa amri kwa hasira na ghadhabu, waletwe hao Shadraka, na Meshaki, na Abednego. Basi wakawaleta watu hao mbele ya mfalme. Nebukadreza akajibu, akawaambia, Enyi Shadraka, na Meshaki, na Abednego, je! Ni kwa makusudi hata hammtumikii mungu wangu wala kuisujudia sanamu ya dhahabu niliyoisimamisha? Basi sasa, kama mkiwa tayari wakati mtakapoisikia sauti ya panda, na filimbi, na kinubi, na zeze, na santuri, na zomari, na namna zote za ngoma, kuanguka na kuisujudia sanamu niliyoisimamisha, ni vema; bali msipoisujudia, mtatupwa saa iyo hiyo katika tanuru iwakayo moto; naye ni nani Mungu yule atakayewaokoa ninyi na mikono yangu? Ndipo Shadraka, na Meshaki, na Abednego, wakajibu, wakamwambia mfalme, Ee Nebukadreza, hamna haja kukujibu katika neno hili. Kama ni hivyo, Mungu wetu tunayemtumikia aweza kutuokoa na tanuru ile iwakayo moto; naye atatuokoa na mkono wako, Ee mfalme. Bali kama si hivyo, ujue, Ee mfalme, ya kuwa sisi hatukubali kuitumikia miungu yako, wala kuisujudia hiyo sanamu ya dhahabu uliyoisimamisha.Ndipo Nebukadreza akajaa ghadhabu, na sura ya uso wake ikabadilika juu ya Shadraka, na Meshaki, na Abednego, basi akatoa amri watie moto ile tanuru mara saba kuliko desturi yake ya kutiwa moto. Kisha akawaamuru baadhi ya watu mashujaa wa jeshi lake kuwafunga Shadraka, na Meshaki, na Abednego, na kuwatupa katika ile tanuru iliyokuwa ikiwaka moto. Basi watu hao wakafungwa, hali wamevaa suruali zao, na kanzu zao, na joho zao, na mavazi yao mengine, wakatupwa katikati ya ile tanuru iliyokuwa ikiwaka moto. Basi kwa sababu amri ya mfalme ilikuwa ni kali, na ile tanuru ilikuwa ina moto sana, mwako wa ule moto ukawaua wale watu waliowashika Shadraka, na Meshaki, na Abednego. Na watu hao watatu, Shadraka, na Meshaki, na Abednego, wakaanguka, hali wamefungwa, katikati ya ile tanuru iliyokuwa inawaka moto. Ndipo Nebukadreza akastaajabu, akainuka kwa haraka; akanena, akawaambia mawaziri wake, Je! Hatukutupa watu watatu, hali wamefungwa, katikati ya moto? Wakajibu, wakamwambia mfalme, Kweli, Ee mfalme. Akajibu, akasema, Tazama, mimi naona watu wanne, nao wamefunguliwa, wanatembea katikati ya moto hali hawana dhara; na sura yake yule wa nne ni mfano wa mwana wa miungu. Kisha Nebukadreza akaukaribia mdomo wa ile tanuru iliyokuwa inawaka moto. Akanena, akasema, Enyi Shadraka, na Meshaki, na Abednego, watumishi wa Mungu Aliye juu, tokeni, mje huku. Ndipo Shadraka, na Meshaki, na Abednego, wakatoka katika ule moto. Na maamiri, na manaibu, na maliwali, na mawaziri, waliokuwa wamekusanyika pamoja, wakawaona watu hao, ya kuwa ule moto ulikuwa hauna nguvu juu ya miili yao, wala nywele za vichwa vyao hazikuteketea, wala suruali zao hazikubadilika, wala harufu ya moto haikuwapata hata kidogo. Nebukadreza akanena, akasema, Na ahimidiwe Mungu wa Shadraka, na Meshaki, na Abednego; aliyemtuma malaika wake, akawaokoa watumishi wake waliomtumaini, wakaligeuza neno la mfalme, na kujitoa miili yao ili wasimtumikie mungu mwingine, wala kumwabudu, ila Mungu wao wenyewe. Basi mimi naweka amri ya kuwa kila kabila ya watu, na kila taifa, na kila lugha, watakaonena neno lo lote lisilopasa juu ya huyo Mungu wa Shadraka, na Meshaki, na Abednego, watakatwa vipande vipande, na nyumba zao zitafanywa jaa; kwa kuwa hakuna Mungu mwingine awezaye kuokoa namna hii.”



Hakikisha kuwa unafanya sehemu yako, unapambana, na Mungu atakusaidia, tambua ya kuwa una kitu cha ziada, na usisubiri mwanadamu akutetee, mtegemee Mungu mwangalie yeye, kumbuka ya kuwa una kitu cha ziada, usikubali kwa namna yoyote ile kupoteza ulichonacho kwa njia rahisi, Pambana kwa kumtegemea Mungu yeye aliyekuweka! Mshike Yesu tu yeye ndio msaada wetu mkubwa na anayeweza kutusaidia usiwategemee wanadamu.

Rev. Innocent Samuel Kamote

Mkuu wa wajenzi mwenye hekima!