1Samuel 17:38-40. “Ndipo Sauli akamvika
Daudi mavazi yake ya vita, akamtia chapeo cha shaba kichwani, akamvika dirii.
Naye Daudi akajifunga upanga juu ya mavazi yake, akajaribu kwenda; maana
alikuwa hajavijaribu. Daudi akamwambia Sauli, Siwezi kwenda na vitu hivi, maana
sikuvijaribu. Basi Daudi akavivua. Akaichukua fimbo yake mkononi, akajichagulia
mawe laini matano katika kijito cha maji, akayatia katika mfuko wa kichungaji
aliokuwa nao, maana ni mkoba wake, na kombeo lake alikuwa nalo mkononi mwake,
akamkaribia yule Mfilisti.”
Utangulizi:
Ni muhimu kufahamu kuwa katika
maisha yetu duniani wakati mwingine adui zetu watatulazimisha kuingia katika
vita hata kama sisi ni watu wa Amani, na ni muhimu kwetu kujua kuwa sisi ni
askari wa Yesu Kristo kwa hiyo tuwapo duniani tunapigana, tunapigana vita vita
inayoonekana na isiyoonekana na kwa sababu hiyo ni lazima kila mmoja wetu
apigane vita vilivyo vizuri na kuilinda Imani, Paulo mtume alipokuwa
anahitimisha kazi yake ya injili duniani alitoa taarifa kuwa amevipiga vita
vizuri.
2Timotheo 4:7-8 “Nimevipiga vita vilivyo
vizuri, mwendo nimeumaliza, Imani nimeilinda; baada ya hayo nimewekewa taji ya
haki, ambayo Bwana, mhukumu mwenye haki, atanipa siku ile; wala si mimi tu, bali
na watu wote pia waliopenda kufunuliwa kwake.”
Katika vita zetu duniani ni
lazima tuelewe kuwa Mungu ndiye anayetufundisha vita na kwa sababu hiyo ni
muhimu kwetu kuwa makini na kujifunza kutoka kwake namna na jinsi tunavyoweza
kupigana vita hizo ili tuweze kushinda.
2Samuel 22:33-35 “Mungu ndiye ngome yangu
yenye nguvu; Naye huwaongoza wakamilifu katika njia yake. Huifanya miguu yangu
kuwa kama ya kulungu; Na kunisimamisha mahali pangu pa juu. Ananifundisha
mikono yangu vita; Hata mikono yangu yaupinda upinde wa shaba.”
Zaburi 18:31-34 “Maana ni nani aliye Mungu
ila Bwana? Ni nani aliye mwamba ila Mungu wetu? Mungu ndiye anifungaye mshipi
wa nguvu, Naye anaifanya kamilifu njia yangu. Miguu yangu anaifanya kuwa ya
kulungu, Na kunisimamisha mahali pangu pa juu. Ananifundisha mikono yangu vita,
Mikono yangu ikaupinda upinde wa shaba.”
Zaburi 144:1-2 “Na ahimidiwe Bwana, mwamba
wangu, Anifundishaye mikono yangu vita, Vidole vyangu kupigana. Mhisani wangu
na boma langu, Ngome yangu na mwokozi wangu, Ngao yangu niliyemkimbilia,
Huwatiisha watu wangu chini yangu.”
Mungu huwafundisha watu wake vita
na namna ya kupigana kwa jina la Bwana na kupata ushindi katika maisha yetu,
Moja ya watu waliokuwa na uhodari katika vita ni pamoja na Daudi na watakatifu
waliotutangulia wao walikuwa hodari katika vita kwa sababu Mungu aliwafundisha
namna ya kupigana kwa usahihi katika maisha haya ya mapigano dhidi ya adui yetu
mkuu ambaye ni shetani, maandiko yanawataja kuwa walikuwa hodari katika vita,
sisi nasi Mungu na atupe kuwa hodari katika vita sawasawa na mapenzi yake
katika jina la Yesu Kristo Mwana wa Mungu aliye hai
Waebrania 11:32-33 “Nami niseme nini tena?
Maana wakati usingenitosha kuleta habari za Gideoni na Baraka na Samsoni na
Yeftha na Daudi na Samweli na za manabii; ambao kwa imani walishinda milki za
wafalme, walitenda haki, walipata ahadi, walifunga vinywa vya simba, walizima
nguvu za moto, waliokoka na makali ya upanga. Walitiwa nguvu baada ya kuwa
dhaifu, walikuwa hodari katika vita, walikimbiza majeshi ya wageni.”
Leo tutachukua muda kujifunza
kutoka kwa Daudi jinsi Mungu alivyoweza kumtumia kuleta ushindi mkubwa kwa watu
wa Taifa lake dhidi ya wafilisti kwa kutumia silaha duni na dhaifu maarufu kama
kombeo, na tutajifunza somo hili Kombeo
la Daudi kwa kuzingatia vipengele vitatu vifuatavyo;-
·
Ufahamu
kuhusu Kombeo
·
Kombeo la
Daudi
·
Kanisa na
kombeo la Daudi.
Ufahamu kuhusu Kombeo.
Mojawapo ya silaha ya zamani sana
ambayo ilitengenezwa kwa kamba zilizofumwa vizuri au ngozi na kuwekewa kifuko
cha ngozi katikati kwaajili ya kuwekea jiwe kisha kuzungushwa na kuliachia jiwe
kwa kasi kubwa na kwa ufundi wa kulenga shabaha ni pamoja na kombeo, Kombeo
kama silaha iliyotumiwa na Daudi kuleta ushindi dhidi ya Goliath sasa ina umri
wa miaka kama 3000, silaha hiyo
maarufu kwa lugha ya kiebania kama “Kela
David” au “Qela David” na kwa kiingereza “David
Sling” Kiswahili inaweza kuitwa “Kombeo
la Daudi” au “Manati ya Daudi”,
ni silaha duni na ya zamani sana iliyotumiwa na watu masikini wasiokuwa na
uwezo hata wa kununua panga au mkuki, ndiyo silaha iliyotumiwa na Daudi kumuua
Goliathi kwa jina la Bwana wa majeshi Mungu wa Israel, jina lingine la kombeo
ni teo.
1Samuel 17:43-45 “Mfilisti akamwambia
Daudi, Je! Mimi ni mbwa hata umenijia kwa fimbo? Mfilisti akamlaani Daudi kwa miungu
yake.Mfilisti akamwambia Daudi, Njoo huku kwangu; nyama yako nitawapa ndege wa
angani na wanyama wa mwituni. Ndipo Daudi akamwambia yule Mfilisti, Wewe
unanijia mimi na upanga, na fumo, na mkuki, bali mimi ninakujia wewe kwa jina
la Bwana wa majeshi, Mungu wa majeshi ya Israeli uliowatukana.”
Ni ukweli uliowazi kuwa ushindi wa Daudi dhidi ya Goliath
haukusababishwa na kombeo pekee bali Mungu alihusika nyuma ya ufundi, Imani na
ujasiri wa Daudi, Daudi mwenyewe alikuwa na uelewa kamili kuwa Bwana angemtia
Goliath katika mikono yake akiwa na uhakika kuwa Mungu haokoi kwa upanga wala
mkuki bali kwa nguvu zake.
1Samuel 17:45-47 “Ndipo Daudi akamwambia
yule Mfilisti, Wewe unanijia mimi na upanga, na fumo, na mkuki, bali mimi
ninakujia wewe kwa jina la Bwana wa majeshi, Mungu wa majeshi ya Israeli
uliowatukana. Siku hii ya leo Bwana atakuua mkononi mwangu, nami nitakupiga, na
kukuondolea kichwa chako, nami leo nitawapa ndege wa angani na wanyama wa nchi
mizoga ya majeshi ya Wafilisti, ili kwamba dunia nzima wajue ya kuwa yuko Mungu
katika Israeli. Nao jamii ya watu wote pia wajue ya kwamba Bwana haokoi kwa
upanga wala kwa mkuki; maana vita ni vya Bwana, naye atawatia ninyi mikononi
mwetu.”
Maneno haya ya Daudi yanathibitisha kuwa kulikuwa na
zaidi ya kombeo katika vita ile, watu wakati mwingine tunaweza kusema kuwa
kombeo la Daudi pia linaweza kuitwa “kombeo
la Bwana”, Mungu alihusika kwa asilimia zote kusababisha muujiza ule
kupitia silaha duni na ya chini na ya kimasikini sana, Wakristo wakati mwingine
tumepambana na maswala magumu sana duniani, na wakati mwingine na watu wakubwa
sana wenye nguvu, wenye akili, wenye
utajiri na uwezo, wasemaji wazuri kuliko sisi lakini tunaweza kuwaangusha chini
kwa silaha zetu duni na zenye kudharaulika endapo tutazitumia silaha hizo vema,
ingawa silaha za vita vyetu si za mwili
lakini tunaelezwa katika maandiko kuwa zina uwezo katika Mungu hata kuangusha
ngome na kila kitu kinachijiinu kinyume na Mungu.
2Wakorintho 10:4-6 “(maana silaha za vita
vyetu si za mwili, bali zina uwezo katika Mungu hata kuangusha ngome ;)
tukiangusha mawazo na kila kitu kilichoinuka, kijiinuacho juu ya elimu ya
Mungu; na tukiteka nyara kila fikira ipate kumtii Kristo; tena tukiwa tayari
kupatiliza maasi yote, kutii kwenu kutakapotimia.”
Pamoja na uduni wa kombeo moja ya
sifa kubwa ya kombeo ilikuwa ni ni silaha ambayo kamwe haiko kwenye kundi la
silaha ya kubahatisha na wale waliojifunza kuitumia wanakiri kuwa inapiga kwa
ustadi na kwa umakini mkubwa, kwa hiyo Daudi alikuwa na uzoefu wa siri wa
matumizi ya silaha hiyo ambayo aliitumia pia kuua dubu na simba kabla ya kujitokeza
hadharani, wapendwa silaha za rohoni kama ukizitumia kwa ustadi zinalenga pale
pale na kumaliza kabisa nguvu za adui bila kubahatisha, Kufunga na kuomba na
matumizi sahihi ya neno la Mungu hakujawai hata siku moja kuwa kitu cha
kubahatisha kama unataka kumpiga adui kwa usahihi basi tumia silaha hizo kwa
usahihi.
Wajibu wa kutokuogopa silaha nzito:
Neno la Mungu limeonya kuwa
hatupaswi kuogopa silaha za upande wa adui hata kama zitaonekana kuwa na ubora
na manufaa kuliko silaha zetu, hatupaswi kuogopa farasi, wala magari ya vita,
wala jeshi kubwa, Mungu amesema katika neno lake havipaswi kuogopewa,
tunapoingia katika uwanja wa vita vya kiroho kamwe tusiogope nguvu za kibinadamu,
wala teknolojia ya vita, wala ufundi wa maneno, wala takwimu ya jeshi kubwa
wala uzoefu na ujuzi wa maadui, Mungu alitaka watu wake wamtegemee yeye tu yeye
mwenyewe ndiye vita yetu, Mungu haokoi kwa wingi,
Kumbukumbu 20:1-4 “Utokapo kwenda vitani kupigana
na adui zako, na kuona farasi, na magari, na watu wengi kuliko wewe,
usiwaogope; kwa kuwa Bwana Mungu wako, yu pamoja nawe, aliyekukweza kutoka nchi
ya Misri. Na iwe, msongeapo mapiganoni, kuhani na akaribie na kusema na watu,
awaambie, Sikizeni, enyi Israeli, hivi leo mwasongea mapiganoni juu ya adui
zenu mioyo yenu na isizime; msiche, wala msiteteme, wala msiingiwe na hofu kwa
ajili ya wao; kwa maana Bwana, Mungu wenu, ndiye awaandamaye kwenda kuwapigania
juu ya adui zenu, ili kuwaokoa ninyi.”
Kumbukumbu 17:16 “Ila asifanye farasi wake
kuwa wengi, wala asiwarudishe watu Misri, ili apate kufanya farasi kuwa wengi;
kwa kuwa Bwana amewaambia, Tangu sasa msirudie tena njia ile.”
Yoshua 11:1-11 “Kisha ikawa, hapo huyo
Yabini, mfalme wa Hazori, aliposikia habari ya mambo hayo, akatuma mjumbe aende
kwa Yobabu, mfalme wa Madoni, na kwa mfalme wa Shimroni, na mfalme wa Akshafu,
na hao wafalme waliokuwa upande wa kaskazini, katika nchi ya vilima, na katika
Araba upande wa kusini wa Kinerethi, na katika Shefela, na katika nchi
zilizoinuka za Dori upande wa magharibi, na kwa Mkanaani upande wa mashariki,
na upande wa magharibi, na kwa Mwamori, na Mhiti, na Mperizi na Myebusi katika
nchi ya vilima, na kwa Mhivi pale chini ya Hermoni katika nchi ya Mispa. Nao wakatoka
nje, wao na jeshi zao zote pamoja nao, watu wengi mno, kama mchanga ulio ufuoni
mwa bahari kwa wingi, pamoja na farasi na magari mengi sana. Wafalme hao wote
wakakutana pamoja; wakaenda na kupanga mahema yao pamoja hapo penye maji ya
Meromu, ili kupigana na Israeli. Bwana akamwambia Yoshua, Usiche wewe kwa ajili
ya hao; kwani kesho wakati kama huu nitawatoa hali wameuawa wote mbele ya
Israeli; utawatema farasi zao, na magari yao utayapiga moto. Basi Yoshua
akaenda, na watu wote wa vita pamoja naye, ili kupigana nao hapo penye maji ya
Meromu ghafula; wakawaangukia. Bwana akawatia mkononi mwa Israeli, nao
wakawapiga, na kuwafukuza hata kufikilia Sidoni ulio mkuu, na hata kufikilia
Misrefoth-maimu, tena hata kufikilia bonde la Mispa upande wa mashariki; wakawapiga
hata wasiwasaze hata mtu mmoja aliyesalia. Yoshua akawafanyia vilevile kama
Bwana alivyomwamuru; akawatema farasi zao, na magari yao akayapiga moto.”
Wakati wote Mungu alifanya vita
na adui za watu wake katika namna ya kushangaza sana, na Mungu aliwaonya watu
wake kutokuzitumainia silaha za kimataifa na za kifalme, aliwataka watu wake
kumtegemea yeye, aliwataka watu wake wawe na ujuzi kuwa sio wingi wa farasi
unaookoa, wala sio wingi wa watu unaookoa wala sio ukubwa wa jeshi, tena
aliwataka hata wasiombe msaada wa kivita kwa majirani hasa Misri na hata wakiteka mateka aliwambia farasi zao wazikate
mishipa na magari yao ya vita wayachome moto, Mungu anajua kuwa ziko silaha
zizisooenakana kwa macho na hata zile zinazoonekana kwa macho na zikadharauliwa
na kuonekana kuwa ni silaha duni, Ni ukweli ulio wazi, kuwa Mungu anazitumia
nyuma ya mambo kufanya mambo makubwa ya kutisha na kushangaza, Mungu hakutaka
watu wajisifie wingi na uwezo wao alitaka watu waelewe na wajue ya kuwa ushindi
unatoka kwa Mungu.
Waamuzi 7:1-2 “Kisha Yerubaali, yaani
Gideoni, na watu wote waliokuwa pamoja naye wakaondoka na mapema, wakapiga
kambi yao karibu na kijito cha Harodi; na kambi ya Midiani ilikuwa upande wao
wa kaskazini, karibu na mlima wa More, bondeni. Bwana akamwambia Gideoni, Watu
hawa walio pamoja nawe ni wengi mno hata nikawatie Wamidiani katika mikono yao,
wasije Israeli wakajivuna juu yangu wakisema, Mkono wangu mwenyewe ndio
ulioniokoa.”
Mungu aliwapunguza wanajeshi
waliotoka na Gideoni kutoka 32,000 hadi
kufikia mia tatu 300 na alimkataza Gideoni kusudi Israel
wasijivunie kuwa ushindi walioupata umetokama na wingi wao, katika vita za
Bwana wingi haumtishi, wala hauhusiki na wokovu wake, Mungu aweza kutumia
silaha duni na watu wachache kusababisha ushindi kwa utukufu wake na kwaajili
ya jina lake ili sifa na utukufu zielekezwe kwake!
Zaburi 33:16-17 “Hapana mfalme aokokaye kwa
wingi wa uwezo, Wala shujaa haokoki kwa wingi wa nguvu. Farasi hafai kitu kwa
wokovu, Wala hamponyi mtu kwa wingi wa nguvu zake.”
Zaburi 20:6-7 “Sasa najua kuwa Bwana
amwokoa masihi wake; Atamjibu kutoka mbingu zake takatifu.Hawa wanataja magari
na hawa farasi, Bali sisi tutalitaja jina la Bwana, Mungu wetu.”
Isaya 31:1-3 “Ole wao watelemkao kwenda
Misri wapate msaada, na kutegemea farasi; watumainio magari kwa kuwa ni mengi,
na wapanda farasi kwa kuwa ni hodari sana; lakini hawamwangalii Mtakatifu wa
Israeli, wala hawamtafuti Bwana! Lakini yeye naye ana akili, naye ataleta uovu,
wala hatayatangua maneno yake; Bali ataondoka juu ya nyumba yao watendao
mabaya, na juu ya msaada wa hao watendao maovu. Basi Wamisri ni wanadamu wala
si Mungu, na farasi zao ni nyama wala si roho; na Bwana atakaponyosha mkono
wake, yeye asaidiaye atajikwaa, na yeye asaidiwaye ataanguka, nao wote pamoja
watakoma.”
Isaya 54:15-17 “Tazama, yamkini
watakusanyana; lakini si kwa shauri langu. Watu wo wote watakaokusanyana juu
yako wataanguka kwa ajili yako.Tazama, nimemwumba mhunzi avukutaye moto wa
makaa, akatoa silaha kwa kazi yake; nami nimemwumba mharibu ili aharibu. Kila
silaha itakayofanyika juu yako haitafanikiwa na kila ulimi utakaoinuka juu yako
katika hukumu utauhukumu kuwa mkosa. Huu ndio urithi wa watumishi wa Bwana, na
haki yao inayotoka kwangu mimi, asema Bwana.”
Kombeo la Daudi
Daudi alikuwa na ujuzi fulani
kuhusu Mungu na maagizo yake katika Torati. Alikuwa amekwisha kujifunza kuwa
Mungu haokoi kwa upanga wala mkuki, alikuwa na ujuzi kuwa Mungu haokoi kwa
kutumia wingi, kwa hiyo alipomwendea adui yake alikuwa na mkoba wa ngozi na
ndani yake alikuwa amekunja kombeo yake na alikuwa na mawe matano laini kutoka
mtoni, yanaitwa mawe laini kwa sababu yalikuwa na uduara flani yaani yasiyoweza
kukata au kuumiza kutokana na kudongoroshwa katika maji, lakini yalikuwa magumu
sana, Wakati Goliath alikuwa na vifaa vya kisasa vya vita, na katika Israel ni mfalme Sauli tu
na mwanae Jonathan ndio waliokuwa na uwezo wa kumiliki upanga, watu wengine
wote walikuwa na silaha duni na za kimasikini, Daudi alikuwa anatambua kuwa
vita ni ya Bwana na kuwa Bwana angewaliwapigania watu wake kwa hiyo Kombeo la
Daudi ilikuwa ni silaha inayoonekana ya
Mungu asiyeonekana, kulikuwa na kitu cha ziada katika kombeo la Daudi, yeye
alionekana ameshika fimbo tu mpaka pale alipoichomoa kombeo lake na kuchagua
jiwe laini na adui alisambaratishwa kwa uwezo wa jina la Bwana kupitia jiwe
lile moja tu kati ya mawe matano aliyokuwa ameyachagua, kwanini Daudi alikuwa
na uhakika wa silaha ile duni kumpa ushindi mkubwa usiokuwa wa kawaida?
-
Daudi alikuwa amefundishwa kupigana, Mungu alimfundisha
Daudi vita na matumizi ya silaha zile duni na zikaonyesha uwezo mkubwa akiwa
nyikani, wakati akiwa anachunga kondoo wa baba yake alikuwa amekwisha kujifunza
kutumia kombeo, na aliona kombeo ikiwashughulikia Dubu na Simba wanyama ambao
ni wakali, aliweza kupambana nao na Mungu akimsaidia, Mungu alimuokoa na
wanyama hao wakali
1Samuel 17:34-37 “Daudi
akamwambia Sauli, Mtumishi wako alikuwa akichunga kondoo za baba yake, na
alipokuwa akija simba, au dubu, akamkamata mwana-kondoo wa lile kundi, mimi
hutoka nikamfuata, nikampiga, nikampokonya kinywani mwake; na akinirukia,
humshika ndevu zake, nikampiga, nikamwua. Mtumishi wako alimwua simba na dubu
pia; na huyu Mfilisti asiyetahiriwa atakuwa kama mmoja wao, kwa sababu
amewatukana majeshi ya Mungu aliye hai. Daudi akasema, Bwana aliyeniokoa na
makucha ya simba, na makucha ya dubu, ataniokoa na mkono wa Mfilisti huyu.
Sauli akamwambia Daudi, Enenda, na Bwana atakuwa pamoja nawe.”
-
Daudi hakutegemea silaha za kifalme, Kulikuwa na
nyakati ambapo wafilisti walihodhi teknolojia ya usindikaji vyuma kwa kusudi la
kuwazuia Waisrael wasitengeneze silaha, hii ilikuwa mbinu ya kimkakati ya adui
ya kuwafanya Israel wawe dhaifu na tegemezi, kwa hiyo watu walioweza kumiliki
silaha za vyuma walikuwa ni wafalme au watu matajiri sana wenye kipato cha hali
ya juu, kwa hiyo mtu kama Daudi hakuwa na uwezo wa kumiliki silaha za chuma
wala hakuwa na ujuzi katika hizo, ilikuwa mtu akitaka kunoa hata jembe ni
lazima aende kwa wafilisti, kwa hiyo uhodari wa vita ulikuwa ni katika matumizi
ya kombeo, fimbo mawe na vifaa vya shambani, wafilisti walitaka kuwanyima
Israel maarifa na dhana za mapigano ili
kujihakikishia ushindi
1Samuel 13:19-22 “Basi,
hakuonekana mhunzi ye yote katika nchi yote ya Israeli; kwa kuwa Wafilisti
walisema, Waebrania wasije wakajifanyizia panga au mikuki; lakini Waisraeli
wote hushuka kwa Wafilisti, ili kunoa kila mtu jembe lake, na mundu wake, na
shoka lake, na sululu yake; ila walikuwa na tupa za kunolea sululu, na miundu,
na mauma, na mashoka; na kwa kuinoa michokoo. Hivyo ikawa, siku ya vita,
haukuonekana mkononi mwa mtu ye yote, miongoni mwa watu waliokuwa pamoja na
Sauli na Yonathani, upanga wala mkuki; isipokuwa Sauli mwenyewe na mwanawe
Yonathani walikuwa navyo.”
-
Daudi alikuwa na ufahamu kuwa vita ni ya Bwana,
Daudi alikuwa na uelewa wa wazi kuwa wao walikuwa na silaha duni, na walinyimwa
teknolojia na hata utengenezaji wa silaha za vita za chuma, watu waliokuwa na
silaha katika Israel ni Sauli na mwanae Jonathani, hivyo Daudi aliweka tumaini
lake lote kwa Mungu, alielewa kuwa kombeo ilikuwa ni silaha duni sana na
haikuwa na mchango wowote kwa mtu ambaye amejivika vyuma mwili mzima lakini
alielewa kuwa Mungu angekuwa nyuma ya kombeo na angeliongoza jiwe kupita popote
palipo wazi hata kama ni kwenye jicho kwani alijifunza kuwa kombeo
lililoongozwa na Bwana halitakosa kulenga shabaha, na mkuki na upanga kama Bwana
hayuko navyo haziwezi kuwa silaha za kutisha kwake, watu waliojifunza kutumia
kombeo au teo walikuwa na uwezo wa kuitumia kwa usahihi sana tangu nyakati za
waamuzi watumiaji wa kombeo walikuwa wanauwezo wa kulenga hata unywele kwa
jiwe na wasikose shabaha kwa hiyo
usahihi wa matumizi ya kombeo ulikuwa wa uhakika kwa kiwango cha juu, sana na
kwa sababu hiyo Daudi hakuidharau silaha yake ndogo na duni akijua kuwa Mungu
ataitumia
1Samuel 17:45 “Ndipo Daudi akamwambia yule Mfilisti,
Wewe unanijia mimi na upanga, na fumo, na mkuki, bali mimi ninakujia wewe kwa
jina la Bwana wa majeshi, Mungu wa majeshi ya Israeli uliowatukana.”
Waamuzi 20:14-16 “Lakini
wana wa Benyamini wakakutanika huko Gibea kutoka katika miji yao, ili watoke
kwenda kupiga vita juu ya wana wa Israeli. Hao wana wa Benyamini walihesabiwa
siku ile kutoka hiyo miji, watu waume ishirini na sita elfu waliotumia upanga,
zaidi ya hao waliokaa Gibea, ambao walihesabiwa watu wateule mia saba. Katika
watu hao wote walikuwako watu waume mia saba waliochaguliwa, wenye shoto; kila
mmoja alikuwa anaweza kuutupia unywele mawe kwa teo, wala asikose.”
Ni kutokana na
umahiri wa silaha hii leo hii Idara ya ulinzi ya Israel Israel Defense Force (IDF) wameendeleza silaha ya kisasa kabisa
inayoitwa kwa jina hili la kombel la Daudi “David’s Sling” ambayo ilianza kutumika kijeshi mwaka 2017 ikiwa na
uwezo wa kuingilia kati na kuharibu mifumo ya ushambuliaji ya maadui kama
wakitumia ndege, drones, na mabomu ya mashambulizi ya kisasa Ballistics missiles za uwezo wa aina
mbalimbali kuanzia kilomita 40 mpaka 300 katika mifumo ya kivita ya kisasa ya
israel
Kanisa na kombeo la Daudi.
Mungu katika mpango wake hata leo
bado ameendelea kulifundisha kanisa lake na kulihimiza, kuendelea kuweka
tumaini letu kwake katika maeneo yote, Pamoja na maendeleo ya kitaaluma na
teknolpojia iliyoko leo na mpanuko mkubwa wa elimu Bado Mungu anataka tumpe
yeye kipaumbele na katika nguvu zake na hekima ya Mungu kuliko nyenzo za kisasa
zilizoko duniani, kuhudumu kwetu na kufundisha kwetu na kuhubiri kwetu kamwe
kusiangukie katika hekima ya kibinadamu bali tuendelee kuzitegemea nguvu za
Mungu katika maisha yetu yote Paulo mtume alikuwa msomi, mwanasheria mkubwa na
mwanafalsafa aliyebobea hata hivyo, alimtegemea sana Mungu katika huduma yake
kuliko Elimu yake na uwezo wake wa
kushawishi, Mungu hutumia Imani yetu
katika jina lake na upako hata kuliko
vyeti vyetu vya kitaaluma, sio vibaya kuwa na taaluma lakini tusisahahu upako
una sehemu muhimu katika maisha yetu ya huduma na utumishi, jumbe zangu zote
zinatokana na muongozo wa Roho Mtakatifu kwanza kisha taaluma hufuata baadae
katika maandalizi, lakini Mungu Roho Mtakakatifu ni namba moja kwangu.
1Wakorintho 2:4-5 “Na neno langu na
kuhubiri kwangu hakukuwa kwa maneno ya hekima yenye kushawishi akili za watu,
bali kwa dalili za Roho na za nguvu, ili imani yenu isiwe katika hekima ya
wanadamu, bali katika nguvu za Mungu.”
Paulo mtume alikuwa na ujuzi ya
kuwa Mungu anaweza kuwatumia wenye cheo na wenye hekima ya dunia hii, lakini
alitahadharisha kuwa Mungu huyatumia mambo manyonge na madhaifu na
yaliyodharauliwa, na wadhaifu, kwa sababu Mungu hataki watu wajisifie mbele
zake kwa sababu ya uwezo wa kibinadamu, bali kwaajili ya jina lake.
1Wakorintho 1:26-29 “Maana, ndugu zangu,
angalieni mwito wenu, ya kwamba si wengi wenye hekima ya mwilini, si wengi
wenye nguvu, si wengi wenye cheo walioitwa; bali Mungu aliyachagua mambo
mapumbavu ya dunia awaaibishe wenye hekima; tena Mungu alivichagua vitu dhaifu
vya dunia ili aviaibishe vyenye nguvu; tena Mungu alivichagua vitu vinyonge vya
dunia na vilivyodharauliwa, naam, vitu ambavyo haviko, ili avibatilishe vile
vilivyoko; mwenye mwili awaye yote asije akajisifu mbele za Mungu.”
Paulo alikuwa na ujuzi ya kuwa
Mungu anaweza kumtumia mtu kwa rehema zake na neema yake tu na ya kuwa juhudi
za kibinadamu haina mchango wowote katika kutupatia kibali cha Mungu, wala
jitidaha za kibinadamu hazina mchango wa kuleta rehema za Mungu kwetu wala
matakwa yetu
Warumi 9:10-16 “Wala si hivyo tu, lakini
Rebeka naye, akiisha kuchukua mimba kwa mume mmoja, naye ni Isaka, baba yetu,(kwa
maana kabla hawajazaliwa wale watoto, wala hawajatenda neno jema wala baya, ili
lisimame kusudi la Mungu la kuchagua, si kwa sababu ya matendo, bali kwa sababu
ya nia yake aitaye), aliambiwa hivi, Mkubwa atamtumikia mdogo. Kama
ilivyoandikwa, Nimempenda Yakobo, bali Esau nimemchukia.Tuseme nini basi? Kuna
udhalimu kwa Mungu? Hasha! Maana amwambia Musa, Nitamrehemu yeye nimrehemuye,
nitamhurumia yeye nimhurumiaye. Basi, kama ni hivyo, si katika uwezo wa yule
atakaye, wala wa yule apigaye mbio; bali wa yule arehemuye, yaani, Mungu.”
Neno la Mungu linatufundisha kuwa
kuna namna ambapo Mungu asipohusika kwenye jambo lolote hata tujihusishe vipi
jambo hilo haliwezi kuwa na maanikio bila ya mkono wake na
jambo hili ndio liko kwenye siri ya kombeo la Daudi
Zaburi 127:1 “Bwana asipoijenga nyumba
Waijengao wafanya kazi bure. Bwana asipoulinda mji Yeye aulindaye akesha bure.”
Yohana 15:4-5 “Kaeni ndani yangu, nami
ndani yenu. Kama vile tawi lisivyoweza kuzaa peke yake, lisipokaa ndani ya
mzabibu; kadhalika nanyi, msipokaa ndani yangu. Mimi ni mzabibu; ninyi ni
matawi, akaaye ndani yangu nami ndani yake, huyo huzaa sana; maana pasipo mimi
ninyi hamwezi kufanya neno lo lote.”
Tunajifunza kuacha kuzitegemea
Pesa kuliko Mungu kuingilia kati maswala yetu, kuacha kutegemea miundo mbinu
bila kumruhusu Roho Mtakatifu katika shughuli zetu, kuacha kutegemea wingi wa
watu kuliko uwepo wa Mungu, tulitegemee neno la Mungu kama upanga wa roho
kwaajili ya ushindi katika maisha yetu, tuyategemee maombi yetu kuleta matokeo
kuliko akili zetu na tumtegemee Mungu kwa Imani hata katika mambo madogo
yasiyotatrajiwa, tutumie kile ambacho Mungu amekiweka ndani yetu kwa utukufu
wake na tunataona ushindi mkubwa katika maisha yetu na hilo ndio kombeo la Daudi, Bila uwepo wa Mungu
kombeo lisingeweza kuwa sababu ya ushindi wa Daudi.
Na Rev. Innocent Samuel Kamote
Mkuu wa wajenzi mwenye Hekima.


