Jumapili, 1 Februari 2026

Nyota za Abrahamu!


Mwanzo 15:1-5. “Baada ya mambo hayo neno la BWANA likamjia Abramu katika njozi, likinena, Usiogope, Abramu, Mimi ni ngao yako, na thawabu yako kubwa sana. Abramu akasema, Ee Bwana MUNGU, utanipa nini, nami naenda zangu hali sina mtoto, na atakayeimiliki nyumba yangu ni huyu Eliezeri, Mdameski? Abramu akasema, Tazama, hukunipa uzao, na mtu aliyezaliwa nyumbani mwangu ndiye mrithi wangu. Nalo neno la BWANA likamjia likinena, Huyu hatakurithi, bali atakayetoka katika viuno vyako ndiye atakayekurithi. Akamleta nje, akasema, Tazama sasa mbinguni, kazihesabu nyota, kama ukiweza kuzihesabu. Akamwambia, Ndivyo utakavyokuwa uzao wako.”




Utangulizi:

Katika aya tulizosoma hapo juu, tunataarifiwa kuwa Mungu alimtembelea Abrahamu katika njozi na kumpa maneno ya kutia moyo, wakati huu Abrahamu alikuwa hana mtoto bado na umri wake ulikuwa umeenda sana na mke wake pia alikuwa mzee, na sasa anawaza kuacha urithi wake kwa Eliezeri mtumishi wake, kimsingi Abrahamu alikuwa amekata tamaa, na Mungu alikuja kumpasha habari za muhimu sana ambazo zilikuwa zinapita uwezo wa kufikiri kwake, wakati Abrahamu alikuwa anafikiri juu ya mtoto mmoja tu, Mungu alikuwa anafikiri uzao mwingi sana kama nyota za angani, Yeye alimleta Abrahamu nje na kumpa kazi ya kuzihesabu nyota na kisha alimhakikishia kuwa ndivyo utakavyokuwa uzao wake! Ahadi hii ya kipekee inazungumzia kuzidishwa kusikoweza kuhesabika, wema na kibali kikubwa sana cha Mungu kwa Abrahamu, na urithi wa kiroho usio na mipaka na hivyo kama wewe ni mtoto wa Abraham kwa ahadi na kwa imani maono haya yanaashiria kuwa wewe sio wa kawaida kama unavyoweza kudhani na Baraka za Mungu kwako hazina mipaka na kuwa hauko duniani kwa hasara, una ushawishi mkubwa na uwepo wako unachangia kitu Fulani duniani, wewe ni nuru inayong’aa gizani, umeinuliwa juu sana wewe si wa kawaida, maono haya hayaleti ujumbe wa uzao tu kwa Abrahamu bali pia yanaleta ujumbe kwetu kuwa sisi ni watoto wa namna gani katika uhusiano wetu na Mungu ona  

1Petro 2:9-10 “Bali ninyi ni mzao mteule, ukuhani wa kifalme, taifa takatifu, watu wa milki ya Mungu, mpate kuzitangaza fadhili zake yeye aliyewaita mtoke gizani mkaingie katika nuru yake ya ajabu; ninyi mliokuwa kwanza si taifa, bali sasa ni taifa la Mungu; mliokuwa hamkupata rehema, bali sasa mmepata rehema.”

Wafilipi 2:14-15. “Yatendeni mambo yote pasipo manung'uniko wala mashindano, mpate kuwa wana wa Mungu wasio na lawama, wala udanganyifu, wasio na ila kati ya kizazi chenye ukaidi, kilichopotoka; ambao kati ya hao mnaonekana kuwa kama mianga katika ulimwengu,”

Leo basi tutachukua muda wetu kujifunza kile Mungu anazungumza na Abrahamu kutuhusu sisi pamoja na wana wa Abrahamu wengineo na kile ambacho Mungu alikuwa anamaanisha katika ujumbe wake kwa Abrahamu na kwetu tutajifuza somo hili “Nyota za Abrahamu” kwa kuzingatia vipengele muhimu vitatu vifuatavyo:-


·         Maana ya Nyota za Abrahamu

·         Nyota za Abrahamu

·         Jinsi ya kuwa nyota za Abrahamu

 

Maana ya Nyota za Abrahamu.

Mwanzo 15:1-5. “Baada ya mambo hayo neno la BWANA likamjia Abramu katika njozi, likinena, Usiogope, Abramu, Mimi ni ngao yako, na thawabu yako kubwa sana. Abramu akasema, Ee Bwana MUNGU, utanipa nini, nami naenda zangu hali sina mtoto, na atakayeimiliki nyumba yangu ni huyu Eliezeri, Mdameski? Abramu akasema, Tazama, hukunipa uzao, na mtu aliyezaliwa nyumbani mwangu ndiye mrithi wangu. Nalo neno la BWANA likamjia likinena, Huyu hatakurithi, bali atakayetoka katika viuno vyako ndiye atakayekurithi. Akamleta nje, akasema, Tazama sasa mbinguni, kazihesabu nyota, kama ukiweza kuzihesabu. Akamwambia, Ndivyo utakavyokuwa uzao wako.”

Ni muhimu kufahamu kuwa asili ya ndoto hii ambayo Mungu alisema na Abrahamu ina uhusiano mkubwa na watoto wa Abrahamu wa kiroho zaidi kuliko watoto wa Abrahamu wa kimwili, kumbuka kuwa hii ilikuwa ni mara nyingine tena zaidi Mungu akizungumza na Abrahamu kuhusu uzao, hasa kwa sababu ya hali yake ya kutokuwa na watoto, Mungu alizungumza kwa namna mbili tofauti na ni lazima namna zote mbili tuzielewe vema, anapozungumza na Abrahamu kuhusu uzao mwingi na uzao wa kimwili au kibaiolojia Mungu anamwambia Abrahamu kuwa uzao wako utakuwa mwingi kama Mchanga au kama mavumbi ya nchi!

Mwanzo 13:14-18 “BWANA akamwambia Abramu, alipokwisha kutengana na Lutu, Inua sasa macho yako, ukatazame kutoka hapo ulipo, upande wa kaskazini, na wa kusini na wa mashariki na wa magharibi;maana nchi hii yote uionayo, nitakupa wewe na uzao wako hata milele.Na uzao wako nitaufanya uwe kama mavumbi ya nchi; hata mtu akiweza kuyahesabu mavumbi ya nchi, uzao wako nao utahesabika. Ondoka, ukatembee katika nchi hii katika mapana yake, na marefu yake, maana nitakupa wewe nchi hiyo. Basi Abramu akajongeza hema yake, akaja akakaa kwenye mialoni ya Mamre, nayo ni miti iliyoko Hebroni, akamjengea BWANA madhabahu huko.”

Hesabu 23:8-10 “Nimlaanije, yeye ambaye Mungu hakumlaani? Nimshutumuje, yeye ambaye Bwana hakumshutumu? Kutoka kilele cha majabali namwona; Na kutoka milimani namtazama; Angalia, ni watu wakaao peke yao, Wala hawatahesabiwa pamoja na mataifa. Ni nani awezaye kufanya idadi ya mavumbi ya Yakobo, Au kuhesabu robo ya Israeli? Na nife kifo chake mwenye haki, Na mwisho wangu uwe mfano wa mwisho wake.”     

Mwanzo 32:10-12 “mimi sistahili hata kidogo hizo rehema zote na kweli yote uliyomfanyia mtumwa wako; maana nalivuka mto huo wa Yordani na fimbo yangu tu, na sasa nimekuwa matuo mawili.Uniokoe sasa na mkono wa ndugu yangu, mkono wa Esau, maana mimi namwogopa, asije akanipiga, na mama pamoja na wana. Nawe ulisema, Hakika nitakutendea mema, nami nitafanya uzao wako uwe kama mchanga wa bahari, usiohesabika kwa kuwa mwingi.”           

Mungu anazungumza na Abrahamu katika fungu hili akumuahidi watoto wa mwilini, wale watakaoirithi nchi pale mashariki ya kati, watoto hawa wanawakilishwa na mavumbi ya nchi, mchanga au mchanga wa bahari, na hapo katika lugha za kinabii wanazungumziwa watoto wa Abrahamu wa kimwili wa kidunia  wanaweza kuwa Wayahudi na Waarabu wa kawaida wasiookoka, kwa hiyo tunafunuliwa hapa katika maandiko kuwa Abrahamu ana watoto wa aina mbili wa mwilini na watoto wa kiroho, au waliozaliwa kwa mwili na wale waliozaliwa kwa Ahadi, tunafahamu kuwa baada ya kifo cha Sara Abraham alikuwa na watoto wengine kupitia Ketura ambao ni Zimran. Yokshan, Medani, Midiani Ishbaki na Shua ambao wengi wanaunda falme za kiarabu mashariki ya kati hata hivyo Ishamel na Isaka ndio wanaotumika zaidi kitheolojia kutufunza watoto hao wa aina mbili wa Abrahamu, yaani mmoja wa mwilini na mwingine wa ahadi, mmoja wa mjakazi na mwingine wa Muungwana, sasa hawa wanawakilishwa na mavumbi na nyota, mavumbi ni wale wa mwilini na Nyota ni wale wa Rohoni, au wa ahadi.

Wagalatia 4:22-23 “Kwa maana imeandikwa ya kuwa, Ibrahimu alikuwa na wana wawili mmoja kwa mjakazi, na mmoja kwa mwungwana. Lakini yule wa mjakazi alizaliwa kwa mwili, yule wa mwungwana kwa ahadi.”

Kwa hiyo maana ya maono ya nyota za Abrahamu hapo, wanazungumziwa watoto wa kiroho wa Abrahamu wana wa ahadi, wale wanaomwamini Mungu kama Abrahamu alivyomwamini Mungu akahesabiwa kuwa na haki, hawa ni wale waliookoka waliomwamini Yesu kama Bwana na mwokozi kutoka kila mahali duniani wawe ni Wayahudi au Wayunani vyovyote kama wamemuamini Bwana Yesu kwa imani hao ni wana wa Ibrahimu wanaotajwa kama nyota

Wagalatia 3:6-9 “Kama vile Ibrahimu alivyomwamini Mungu akahesabiwa haki.Fahamuni basi, ya kuwa wale walio wa imani, hao ndio wana wa Ibrahimu.Na andiko, kwa vile lilivyoona tangu zamani kwamba Mungu atawahesabia haki Mataifa kwa imani, lilimhubiri Ibrahimu habari njema zamani, kusema, Katika wewe Mataifa yote watabarikiwa. Basi hao walio wa imani hubarikiwa pamoja na Ibrahimu aliyekuwa mwenye imani.”

Kwa hiyo Mungu anapozungumza na Abrahamu kwa habari ya watoto wa Mwilini anamuahidi uzao kama mavumbi ya nchi na anapozungumza naye kuhusu watoto wa kiroho anazungumza na Abrahamu kwa ahadi ya kuhesabia nyota, kwa hiyo nyota za Abrahamu ni watoto wake wa kiroho yaani wewe na mimi tuliookoka tulio mwamini Yesu na kuhesabiwa haki kwa imani sisi ndio “Nyota za Abrahamu” kwa hiyo katika ahadi ya uzao kwa Ibrahimu kumbuka kuna uzao kama nyota za angani na uzao kama mchanga wa bahari au mavumbi ya nchi hii inatofautisha watoto wa mwilini na watoto wa rohoni  wa Ibrahimu mwenye kusikia na asikie! Mungu anaahidi kuwabariki watoto hao wote

Mwanzo 22:16-18. “akasema, Nimeapa kwa nafsi yangu asema BWANA, kwa kuwa umetenda neno hili, wala hukunizuilia mwanao, mwanao wa pekee, katika kubariki nitakubariki, na katika kuzidisha nitauzidisha uzao wako KAMA NYOTA ZA MBINGUNI, na KAMA MCHANGA ULIOKO PWANI; na uzao wako utamiliki mlango wa adui zao; na katika uzao wako mataifa yote ya dunia watajibarikia; kwa sababu umetii sauti yangu.”

Nyota za Abrahamu.

Mwanzo 15:1-5. “Baada ya mambo hayo neno la BWANA likamjia Abramu katika njozi, likinena, Usiogope, Abramu, Mimi ni ngao yako, na thawabu yako kubwa sana. Abramu akasema, Ee Bwana MUNGU, utanipa nini, nami naenda zangu hali sina mtoto, na atakayeimiliki nyumba yangu ni huyu Eliezeri, Mdameski? Abramu akasema, Tazama, hukunipa uzao, na mtu aliyezaliwa nyumbani mwangu ndiye mrithi wangu. Nalo neno la BWANA likamjia likinena, Huyu hatakurithi, bali atakayetoka katika viuno vyako ndiye atakayekurithi. Akamleta nje, akasema, Tazama sasa mbinguni, kazihesabu nyota, kama ukiweza kuzihesabu. Akamwambia, Ndivyo utakavyokuwa uzao wako.”

Kimsingi katika maono haya Mungu alikuwa anafanya agano na Abrahamu kuwa atakuwa na watoto wa agano au watoto wa ahadi, au watoto wa imani ambao watakuwa na uwezo mkubwa sana na wenye Baraka za kudumu, watakuwa ni watoto ambao hawawezi kueleweka kwa hesabu za kibinadamu, watakuwa na ushawishi mkubwa duniani, watatoa muelekeo, wataipa dunia nuru, watatofautishwa na giza, wao hawatakuwa wa kawaida, wasioweza kuwekewa mipaka, wasiohesabika, watoto hao ni sisi na uweza wao unaelezewa katika maandiko kwa njia ya kipeke

1.       Ni watoto wa Imani – Abrahamu alikuwa katika mashaka makubwa sana , umri unaenda mkewe amezeeka na anawasiwasi kuhusu warithi wake, Lakini kwa Mungu hiyo haikuwa shida alikuwa amekusudia kumpa Abrahamu watoto wa aina zote watoto wa mwilini na watoto wa rohoni na wote wangekuwa wengi sana wa mwilini kama mchanga wa bahari na wa kiroho au wa Imani kama nyota  za mbinguni ona:-

 

Mwanzo 22:16-18. “akasema, Nimeapa kwa nafsi yangu asema BWANA, kwa kuwa umetenda neno hili, wala hukunizuilia mwanao, mwanao wa pekee,katika kubariki nitakubariki, na katika kuzidisha nitauzidisha uzao wako KAMA NYOTA ZA MBINGUNI, na KAMA MCHANGA ULIOKO PWANI; na uzao wako utamiliki mlango wa adui zao; na katika uzao wako mataifa yote ya dunia watajibarikia; kwa sababu umetii sauti yangu.”

 

Watoto wanaofananishwa na Nyota za mbinguni ni watoto wa kiroho ni watoto wa Imani, hawa sio wale wanaozaliwa kwa damu na nyama bali ni wale wanaozaliwa kwa imani wale waliomwamini Mungu kama Ibrahimu aliyomwamini Mungu na kuhesabiwa kuwa haki.

 

Wagalatia 3:6-9 “Kama vile Ibrahimu alivyomwamini Mungu akahesabiwa haki.Fahamuni basi, ya kuwa wale walio wa imani, hao ndio wana wa Ibrahimu.Na andiko, kwa vile lilivyoona tangu zamani kwamba Mungu atawahesabia haki Mataifa kwa imani, lilimhubiri Ibrahimu habari njema zamani, kusema, Katika wewe Mataifa yote watabarikiwa.Basi hao walio wa imani hubarikiwa pamoja na Ibrahimu aliyekuwa mwenye imani.”

 

2.       Ni watoto wasio na mipaka - Akamleta nje, akasema, Tazama sasa mbinguni, kazihesabu nyota, kama ukiweza kuzihesabu. Akamwambia, Ndivyo utakavyokuwa uzao wako, Mungu alimtoa Abrahamu nje, ilikuwa nje ya hema yake, ilikuwa nje ya kuta za nyumba, ilikuwa nje ya dunia,  ilikuwa nje ya mipaka ya kimazingira, ilikuwa nje ya fikra finyu, inayoishia kwenye anga la dunia, akamwangalisha juu, alimtazamisha mbinguni akamuamuru ahesabie nyota kama ataweza akamwambia ndivyo utakavyokuwa uzao wako, Mungu alikuwa anasema na Abrahamu kuwa wazao wake Nyota za Abrahamu hawatakuwa na mipaka, wala hawawezi kuhesabiwa kwa hesabu za kidunia wala za kibinadamu, mtu yeyote anayetaka kuangalia mambo kwa upana haangalii mambo ya duniani pekee, anaangalia yaliyo juu, watoto wa Abrahamu au nyota za Abrahamu huangalia mambo kwa upana, wanaona mbali, hawaangalii vya muda wanaaangalia vya milele, hawafikri yaliyo katika nchi pekee wanafikiri yaliyo juu, huwezi kuwawekea mipaka watu wenye mtazamo unaozidi mtazamo wa kidunia, nyota hazikai katika anga hili nyota zinakaa mbali ziko juu sana na ni kubwa mno

 

Wakolosai 3:1-2 “Basi mkiwa mmefufuliwa pamoja na Kristo, yatafuteni yaliyo juu Kristo aliko, ameketi mkono wa kuume wa Mungu. Yafikirini yaliyo juu, siyo yaliyo katika nchi.”

 

2Wakorintho 4:16-18. “Kwa hiyo hatulegei; bali ijapokuwa utu wetu wa nje unachakaa, lakini utu wetu wa ndani unafanywa upya siku kwa siku. Maana dhiki yetu nyepesi, iliyo ya muda wa kitambo tu, yatufanyia utukufu wa milele uzidio kuwa mwingi sana; tusiviangalie vinavyoonekana, bali visivyoonekana. Kwa maana vinavyoonekana ni vya muda tu; bali visivyoonekana ni vya milele.

 

3.       Ni watoto wenye wito wa mbinguni – Nyota za Abrahamu ni watoto wa Imani wa Ibrahimu ambao wameitwa na Mungu kwaajili ya wito mkuu wa Mungu wa maisha yasiyokuwa ya kawaida kusudi lao si la kidunia kusudi lao ni la kimbingu, ni watu ambao wenyeji wao uko mbinguni wao wako ulimwenguni lakini sio wa ulimwengu huu,  

 

Waebrania 3:1-2. “Kwa hiyo, ndugu watakatifu, wenye kuushiriki mwito wa mbinguni, mtafakarini sana Mtume na Kuhani Mkuu wa maungamo yetu, Yesu, aliyekuwa mwaminifu kwake yeye aliyemweka, kama Musa naye alivyokuwa, katika nyumba yote ya Mungu.”

 

Wafilipi 3:20-21 “Kwa maana sisi, wenyeji wetu uko mbinguni; kutoka huko tena tunamtazamia Mwokozi, Bwana Yesu Kristo; atakayeubadili mwili wetu wa unyonge, upate kufanana na mwili wake wa utukufu, kwa uweza ule ambao kwa huo aweza hata kuvitiisha vitu vyote viwe chini yake.”

 

Yohana 15:18-19. “Iwapo ulimwengu ukiwachukia, mwajua ya kuwa umenichukia mimi kabla ya kuwachukia ninyi. Kama mngekuwa wa ulimwengu, ulimwengu ungewapenda walio wake; lakini kwa kuwa ninyi si wa ulimwengu, bali mimi naliwachagua katika ulimwengu, kwa sababu hiyo ulimwengu huwachukia.”

 

4.       Ni watoto wenye hekima isiyo ya dunia hii – Watoto wa Abrahamu au nyota za Abrahamu ni wenye kutoa muongozo. Wanatoa nuru na wako tofauti na wana wa giza, tofauti na wana siasa na watawala wa dunia hii hekima waliyonayo wanaitumia kuwavuta wengi na kuwaongoza katika kuishi maisha ya haki, Nyota zinaashiria ushawishi wenye manufaa, zinaashiria uwezo wa juu wa kimtazamo, mawazo  mapana na hekima ya hali ya juu, hekima isiyokuwa ya kawaida, isiyo ya duania hii, hekima iliyohifadhiwa kwaajili yetu tu

 

Daniel 12:3 “Na walio na hekima watang'aa kama mwangaza wa anga; na hao waongozao wengi kutenda haki watang'aa kama nyota milele na milele.”

 

1Wakorintho 2:6-7 “Walakini iko hekima tusemayo kati ya wakamilifu; ila si hekima ya dunia hii, wala ya hao wanaoitawala dunia hii, wanaobatilika; bali twanena hekima ya Mungu katika siri, ile hekima iliyofichwa, ambayo Mungu aliiazimu tangu milele, kwa utukufu wetu;

 

Yakobo 3:15-17 “Hekima hiyo siyo ile ishukayo kutoka juu, bali ni ya dunia, ya tabia ya kibinadamu, na Shetani. Maana hapo palipo wivu na ugomvi ndipo palipo machafuko, na kila tendo baya. Lakini hekima itokayo juu, kwanza ni safi, tena ni ya amani, ya upole, tayari kusikiliza maneno ya watu, imejaa rehema na matunda mema, haina fitina, haina unafiki.”

 

5.       Ni watoto wa Nuru – Nyota zina sifa maalumu na sifa mojawapo ni kung’aa gizani, na hivyo kuziwezesha kung’aa usiku zadi wakati dunia ikiwa giza, dunia inapokuwa imeharibiwa na giza la dhambi, giza la kutokuyajua mapenzi ya Mungu, giza la kutokuona mbele, giza la kutokumfahamu Mungu watoto wa Abrahamu ambao ni nyota huiangaza Dunia hawa ni wana wa Nuru na kamwe sio wana wa giza, kazi yao ni kuleta ufumbuzi, ni kuiangazia dunia isiwe na ukiwa, isiwe na giza, isipoteze ladha  na isiwe yenye kutisha

 

Mathayo 5:14-16 “Ninyi ni nuru ya ulimwengu. Mji hauwezi kusitirika ukiwa juu ya mlima. Wala watu hawawashi taa na kuiweka chini ya pishi, bali juu ya kiango; nayo yawaangaza wote waliomo nyumbani.Vivyo hivyo nuru yenu na iangaze mbele ya watu, wapate kuyaona matendo yenu mema, wamtukuze Baba yenu aliye mbinguni.”

 

1Wathesalonike 5:4-5 “Bali ninyi, ndugu, hammo gizani, hata siku ile iwapate kama mwivi. Kwa kuwa ninyi nyote mmekuwa wana wa nuru, na wana wa mchana; sisi si wa usiku, wala wa giza.”

       

6.       Ni watoto wenye uwezo wa kutangaza fadhili/utukufu wa Mungu – Nyota za Abrahamu maisha yao ni ya ushindi na ushuhuda, tabia zao na matendo yao humtukuza Mungu, na shuhuda zao zinatangaza fadhili za Mungu, Kama jinsi maandiko yasemavyo kuwa moja ya kazi za anga au mbingu ni kuhubiri utukufu wa Mungu hivyo ndivyo uzao wa Abrahamu yaani nyota za Abrahamu hutangaza fadhili na utukufu wa Mungu

 

Zaburi 19:1-4 “Mbingu zauhubiri utukufu wa Mungu, Na anga laitangaza kazi ya mikono yake. Mchana husemezana na mchana, Usiku hutolea usiku maarifa.Hakuna lugha wala maneno, Sauti yao haisikilikani. Sauti yao imeenea duniani mwote, Na maneno yao hata miisho ya ulimwengu. Katika hizo ameliwekea jua hema,”

 

1Petro 2:9-10 “Bali ninyi ni mzao mteule, ukuhani wa kifalme, taifa takatifu, watu wa milki ya Mungu, mpate kuzitangaza fadhili zake yeye aliyewaita mtoke gizani mkaingie katika nuru yake ya ajabu; ninyi mliokuwa kwanza si taifa, bali sasa ni taifa la Mungu; mliokuwa hamkupata rehema, bali sasa mmepata rehema.”

 

7.       Ni watoto wasioweza kurogeka wala kulaanika – Nyota za Abrahamu ni watoto waliobarikiwa ambao nguvu za giza, uchawi na waganga hauwawezi, wao wanalindwa na nguvu za Mungu awaye yote atakayejaribu kufanya lolote la kichawi au la kiganga kwa lengo la kuwadhuru watoto wa Abrahamu wa Imani atashughulikiwa na Mungu mwenyewe. Watoto wa duniani wanaweza kurogwa kwa kuchukua Mchanga wa mbinguni utachukua nini huwezo kuchota nyao za watoto wa mbinguni, huwezi kufukia kitu kwao ukatoboa hawarogeki!

 

Hesabu 23:7-9 “Akatunga mithali yake, akasema, Balaki amenileta kutoka Aramu, Mfalme wa Moabu kutoka milima ya mashariki, Njoo! Unilaanie Yakobo, Njoo! Unishutumie Israeli. Nimlaanije, yeye ambaye Mungu hakumlaani? Nimshutumuje, yeye ambaye Bwana hakumshutumu? Kutoka kilele cha majabali namwona; Na kutoka milimani namtazama; Angalia, ni watu wakaao peke yao, Wala hawatahesabiwa pamoja na mataifa.”

 

Hesabu 23:18-24 “Naye akatunga mithali yake, akasema, Ondoka Balaki, ukasikilize; Nisikilize, Ee mwana wa Sipori; Mungu si mtu, aseme uongo; Wala si mwanadamu, ajute; Iwapo amesema, hatalitenda? Iwapo amenena, hatalifikiliza? Tazama, nimepewa amri kubariki, Yeye amebariki, nami siwezi kulitangua. Hakutazama uovu katika Yakobo, Wala hakuona ukaidi katika Israeli. Bwana, Mungu wake, yu pamoja naye, Na sauti kuu ya mfalme i katikati yao. Mungu amewaleta kutoka Misri, Naye ana nguvu kama nguvu za nyati. Hakika hapana uchawi juu ya Yakobo, Wala hapana uganga juu ya Israeli. Sasa habari za Yakobo na Israeli zitasemwa, Ni mambo gani aliyoyatenda Mungu! Tazama, watu hawa wanaondoka kama simba mke, Na kama simba anajiinua nafsi yake, Hatalala hata atakapokula mawindo, Na kunywa damu yao waliouawa.”

 

8.       Watawashinda adui zao – Hakuna adui atakayeweza kusimama kinyume na Nyota za Abrahamu, Neno la Mungu la kinabii limeahidi ushindi dhidi ya adui wote wanaowazunguka watoto wa Abrahamu, watakata pembe za adui zao, watawavunja vunja wana wote wa ghasia, Uzao huu utamiliki mlango wa adui zao

 

Hesabu 24:16-19 “Asema, yeye asikiaye maneno ya Mungu, Na kuyajua maarifa yake Aliye Juu. Yeye aonaye maono ya Mwenyezi, Akianguka kifudifudi, amefumbuliwa macho, Namwona, lakini si sasa; Namtazama, lakini si karibu; Nyota itatokea katika Yakobo Na fimbo ya enzi itainuka katika Israeli; Nayo itazipiga-piga pembe za Moabu, Na kuwavunja-vunja wana wote wa ghasia. Na Edomu itakuwa milki Seiri pia itakuwa milki, waliokuwa adui zake; Israeli watakapotenda kwa ushujaa.Mwenye kutawala atakuja toka Yakobo, Atawaangamiza watakaobaki mjini.”

Mwanzo 22:16-18. “akasema, Nimeapa kwa nafsi yangu asema BWANA, kwa kuwa umetenda neno hili, wala hukunizuilia mwanao, mwanao wa pekee, katika kubariki nitakubariki, na katika kuzidisha nitauzidisha uzao wako KAMA NYOTA ZA MBINGUNI, na KAMA MCHANGA ULIOKO PWANI; na uzao wako utamiliki mlango wa adui zao; na katika uzao wako mataifa yote ya dunia watajibarikia; kwa sababu umetii sauti yangu.”

                                 

Jinsi ya kuwa nyota za Abrahamu

Ni muhimu kuwa na uelewa na ufahamu kuwa Nyota za Abrahamu sio swala la ndoto na maono ya kawaida Nyota za Abrahamu leo ni mimi na wewe, Nyota za Abrahamu ni wana wa angani ni wana wa ahadi, Abrahamu ana wana wa aina mbili Nyota na Vumbi, wewe mwenyewe unaweza kuchagua kuwa mwana wa Abrahamu kwa maisha yako unaishije? Unaangaza au umefichwa, umefufuka au umezikwa, ni wa chini au ni wa juu wewe ni wa ulimwengu huu au wewe sio wa ulimwengu huu, wewe ni mwana wa Nuru au u mwana wa giza  unaishi kwa Imani au kwa kuona? una mchango duniani kwa kuangaza au huangazi, kama wewe ni mwana wa Abrahamu Nyota za Abrahamu utaenenda kwa Imani na sio kwa kuona, pale ambapo dunia inasema haiwezekani watu wa Mungu wanasema inawezekana, wana wa Abrahamu ni watoto wenye Imani, wanaishi wakimpendeza Mungu kwa Imani, hakuna jambo lenye mipaka Mbinguni, wakiroga mavumbi ya ardhi sisi haturogeki mpaka upande mbinguni, ukituweka kwenye giza tunang’aa,. Sisi ni wana wa ahadi ahatukuzaliwa kwa mwili, sisi ni wa maono ya kimbinguni na sio ya kidunia huwezi kumuwekea mipaka kwa uhuru tulio nao angani, unataka kuwa mwana wa Abrahamu ambaye ni Nyota hapa duniani uokoke leo, unataka kuwa Mwana wa Abrahamu mavumbi usiokoke ukanywagwe duniani.

2Wakorintho 5:7-9 “(Maana twaenenda kwa imani, si kwa kuona.) Lakini tuna moyo mkuu; nasi tunaona ni afadhali kutokuwamo katika mwili na kukaa pamoja na Bwana. Kwa hiyo, tena, ikiwa tupo hapa, au ikiwa hatupo hapa, twajitahidi kumpendeza yeye

Luka 19:8-10 “Zakayo akasimama, akamwambia Bwana, Tazama, Bwana, nusu ya mali yangu nawapa maskini, na ikiwa nimenyang'anya mtu kitu kwa hila namrudishia mara nne.Yesu akamwambia, Leo wokovu umefika nyumbani humu, kwa sababu huyu naye ni mwana wa Ibrahimu. Kwa kuwa Mwana wa Adamu alikuja kutafuta na kuokoa kile kilichopotea.”

Zakayo alikuwa Myahudi, lakini alikuwa uzao wa Abrahamu upande wa mavumbi, lakini alipookolewa Yesu alisema huyu naye ni mwana wa Ibrahimu, ukimkubali Yesu kuanzia leo unakuwa mwana wa Ibrahimu, ukiendelea kung’ang’ania dini kama mafarisayo unapoteza sifa ya kuwa mwana wa Ibrahimu, Wayahudi wengi waligeuka kuwa wana wa Ibilisi na wana wa mavumbi na kamwe hawakuwa nyota ya Abrahamu kwa sababu dini iliwageuza wakawa na roho mbaya na wauaji, wenye kujihesabia haki na wala hawakutenda mapenzi ya Mungu unataka kuwa Nyota za Abrahamu toka gizani leo uje nuruni, Mwombe Mungu uokolewe! Ukiokoka na kumwamini Yesu wewe ni nyota!

Yohana 8:39-44 “Wakajibu, wakamwambia, Baba yetu ndiye Ibrahimu! Yesu akawaambia, Kama mngekuwa watoto wa Ibrahimu, mngezitenda kazi zake Ibrahimu.Lakini sasa mnatafuta kuniua mimi, mtu ambaye nimewaambia iliyo kweli, niliyoisikia kwa Mungu. Ibrahimu hakufanya hivyo. Ninyi mnazitenda kazi za baba yenu. Ndipo walipomwambia, Sisi hatukuzaliwa kwa zinaa; sisi tunaye Baba mmoja, yaani, Mungu. Yesu akawaambia, Kama Mungu angekuwa baba yenu, mngenipenda mimi; kwa maana nalitoka kwa Mungu, nami nimekuja; wala sikuja kwa nafsi yangu, bali yeye ndiye aliyenituma. Mbona hamyafahamu hayo niyasemayo? Ni kwa sababu ninyi hamwezi kulisikia neno langu. Ninyi ni wa baba yenu, Ibilisi, na tamaa za baba yenu ndizo mpendazo kuzitenda. Yeye alikuwa mwuaji tangu mwanzo; wala hakusimama katika kweli, kwa kuwa hamna hiyo kweli ndani yake. Asemapo uongo, husema yaliyo yake mwenyewe; kwa sababu yeye ni mwongo, na baba wa huo.”

Wafilipi 2:14-15. “Yatendeni mambo yote pasipo manung'uniko wala mashindano, mpate kuwa wana wa Mungu wasio na lawama, wala udanganyifu, wasio na ila kati ya kizazi chenye ukaidi, kilichopotoka; ambao kati ya hao mnaonekana kuwa kama mianga katika ulimwengu,”

Rev. Innocent Samuel Kamote

Mkuu wa wajenzi mwenye Hekima!     

Jumatano, 28 Januari 2026

Hatimaye ndugu tuombeeni!


Warumi 15:30-32 “Ndugu zangu, nawasihi kwa Bwana wetu Yesu Kristo, na kwa upendo wa Roho, jitahidini pamoja nami katika maombi yenu kwa ajili yangu mbele za Mungu; kwamba niokolewe na wale wasioamini katika Uyahudi, na tena huduma yangu niliyo nayo huko Yerusalemu ikubalike kwa watakatifu; nipate kufika kwenu kwa furaha, kama apendavyo Mungu, nikapate kupumzika pamoja nanyi.”




Utangulizi:

Ni muhimu kwetu kama kanisa kuwa na ufahamu, kuwa kuna changamoto kubwa katika kanisa la Mungu na changamoto mojawapo  kubwa ni hii ya kutokuwaombea watumishi wa Mungu, changamoto hii inaweza kuwa inachangiwa na ufahamu finyu wa neno la Mungu, au kutokutiliwa mkazo kwa fundisho hili muhimu na la msingi la kuwaombea watumishi wa Mungu, Mtume, Nabii, Mwinjilisti, Mchungaji na Mwalimu asiyekuwa na waombaji kwaajili yake hana tofauti na Askari aliyeingia vitani pake yake, akishambuliwa yeye hakuna tena msaada mwingine, Ni muhimu kuwa na maarifa na ufahamu ya kuwa kila huduma katika ufalme wa Mungu ina vita na mashambulizi mengi  ya upinzani wa ibilisi huelekezwa kwa watumishi wa Mungu, tunapowaombea tunawasaidia katika ulimwengu wa roho kuepushwa na mashambulizi makali na kuwawekea ulinzi dhidi ya utawala wa giza.

Mathayo 26:30-31 “Nao walipokwisha kuimba, wakatoka nje kwenda mlima wa Mizeituni. Ndipo Yesu akawaambia, Ninyi nyote mtachukizwa kwa ajili yangu usiku huu kwa kuwa imeandikwa, Nitampiga mchungaji, na kondoo wa kundi watatawanyika.”

Wakati Mungu amewatenga watumishi wake wawe kama chombo cha kuwakilisha kazi yake duniani, shetani naye anawalenga wawe silaha maalumu ya kuharibu kazi ya Mungu, au anaweza kutumia hila na mbinu mbalimbali kwa kusudi la kuwakwamisha ili kazi ya Mungu asiendelee mbele na ndio maana kwa kujua hali ilivyo katika ulimwengu wa Roho Paulo Mtume mara kwa mara aliwaomba watu wa makanisa mbalimbali wamuombee, tusipokuwa  na watu wa kutuombea katika huduma zetu tunajiweka katika hatari ya vita kali na kukabiliana na mashambulizi ya huduma peke yako, Jambo ambalo linaweza kusababisha ukadhoofika mapema na kuchoka.

2Wathesalonike 3:1-4 “Hatimaye, ndugu, tuombeeni, neno la Bwana liendelee, na kutukuzwa vile vile kama ilivyo kwenu; tukaokolewe na watu wasio haki, wabaya; maana si wote walio na imani. Lakini Bwana ni mwaminifu, atakayewafanya imara na kuwalinda na yule mwovu. Nasi tumemtumaini Bwana kwa mambo yenu, kwamba mnayafanya tulivyowaagiza, tena kwamba mtayafanya.”

Tutajifunza somo hili muhimu Ndugu tuombeeni kwa kuzingatia vipengele vikuu vitatu vifuatavyo:-

 

·         Umuhimu wa kuwaombea watumishi wa Mungu.

·         Hatimaye ndugu tuombeeni.

·         Mifano ya watumishi wa Mungu waliokuwa na timu za waombaji.

 

Umuhimu wa kuwaombea watumishi wa Mungu.

Ni muhimu kuwa na ufahamu na maarifa kuwa watumishi wa Mungu wa aina zote wanahitaji maombi, na sio tu kuombewa  na washirika pekee lakini ikiwa uko uwezekano pia wawe na timu yaani kikundi au watu maalumu ambao wanaifanya kazi hiyo kwa uaminifu, Swala la kuombewa kwa watumishi wa Mungu ni swala la kiroho kabisa, na ni la kibiblia, kuomba maombi kwa washirika wetu ni swala la kibiblia na ni swala la unyenyekevu unaoonyesha kuwa tunahitaji neema ya Mungu baadhi ya watumishi wa Mungu wanafikiri kuomba maombi kwa washirika na kuwa na timu maalumu ya kuwaombea ni kuonyesha udhaifu, Jambo hili sio sahihi Kwani neno la Mungu linaonyesha kuwa watumishi wa Mungu wanahitaji kuombewa, Nyakati za Kanisa la kwanza walipoteza viongozi Muhimu sana wenye uwezo mkubwa sana katika jamii ya Kikristo mpaka walipopata ufunuo wa kuhakikisha kuwa wanaomba kwa nguvu na juhudi kubwa kwaajili ya wachungaji wao.

Matendo 6:8-13 “Na Stefano, akijaa neema na uwezo, alikuwa akifanya maajabu na ishara kubwa katika watu. Lakini baadhi ya watu wa sinagogi lililoitwa sinagogi la Mahuru, na la Wakirene, na la Waiskanderia, na la wale wa Kilikia na Asia, wakaondoka na kujadiliana na Stefano; lakini hawakuweza kushindana na hiyo hekima na huyo Roho aliyesema naye. Hata wakashawishi watu waliosema, Tumemsikia mtu huyu akinena maneno ya kumtukana Musa na Mungu. Wakawataharakisha watu na wazee na waandishi, wakamwendea, wakamkamata, wakampeleka mbele ya baraza. Wakasimamisha mashahidi wa uongo waliosema, Mtu huyu haachi kusema maneno ya kufuru juu ya mahali hapa patakatifu na juu ya torati;”

Matendo 7:57-60 “Wakapiga kelele kwa sauti kuu, wakaziba masikio yao, wakamrukia kwa nia moja, wakamtoa nje ya mji, wakampiga kwa mawe. Nao mashahidi wakaweka nguo zao miguuni pa kijana mmoja aliyeitwa Sauli. Wakampiga kwa mawe Stefano, naye akiomba, akisema, Bwana Yesu, pokea roho yangu. Akapiga magoti, akalia kwa sauti kuu, Bwana, usiwahesabie dhambi hii. Akiisha kusema haya akalala. Na Sauli alikuwa akiona vema kwa kuuawa kwake.”

Matendo 12:1-5 “Panapo majira yale yale Herode mfalme akanyosha mikono yake kuwatenda mabaya baadhi ya watu wa kanisa. Akamwua Yakobo, ndugu yake Yohana, kwa upanga. Na akiona ya kuwa imewapendeza Wayahudi akaendelea akamshika na Petro. Siku hizo zilikuwa siku za mikate isiyochachwa. Alipokwisha kumkamata, akamweka gerezani akamtia mikononi mwa vikosi vinne vya askari wanne wanne, wamlinde, akitaka baada ya Pasaka kumtoa na kumweka mbele ya watu.Basi Petro akalindwa gerezani, nalo kanisa likamwomba Mungu kwa juhudi kwa ajili yake.”

Tunaona jinsi nyakati za kanisa la kwanza shetani alivyowatumia watu waovu kupinga kazi ya Mungu hasa kwa kuwaua viongozi wa kanisa wale waliokuwa mstari wa mbele katika kuieneza kazi ya injili, aliuawa Stefano na pia Yakobo Mtume ndugu yake Yohana, na Petro akakamatwa, ni wazi kabisa huu ulikuwa ni mpango mkakati wa kishetani wa kutaka kulidhoofisha kanisa, kwa hiyo hata kama kanisa lilikuwa linaomba sasa waliongeza kasi ya kumuomba Mungu kwa juhudi kwaajili ya viongozi wengine, tunasoma kuwa hata Petro alikamatwa lakini kanisa lilipoomba kwa juhudi Mungu alimtuma malaika wake na Petro akawekwa huru, tangu wakati huu, viongozi na washirika walielewa kuwa wanapaswa kuwalinda watumishi wa Mungu kwa maombi na kuwaombea ili kazi ya kueneza neema hii iweze kusonga mbele, kazi ya Mungu ina upinzani mkubwa na viongozi ndio wanaowindwa zaidi kwa sababu hiyo ni muhimu sana kwa kanisa kuomba, kuwa na programu endelevu za maombi ya kimkakati kuwaombea watumishi wa Mungu, kazi ya Mungu iweze kuendelea, ishara na miujiza viweze kufanyika, Na neno la Mungu liendelee kuhubiriwa kwa ujasiri.

Matendo 4:21-31“Nao walipokwisha kuwatisha tena wakawafungua, wasione njia ya kuwaadhibu, kwa sababu ya watu; kwa kuwa watu wote walikuwa wakimtukuza Mungu kwa hayo yaliyotendeka; maana umri wake yule mtu aliyefanyiwa ishara hii ya kuponya ulipita miaka arobaini. Hata walipofunguliwa, wakaenda kwa watu wao, wakawapasha habari ya mambo yote waliyoambiwa na wakuu wa makuhani na wazee. Nao waliposikia, wakampazia Mungu sauti zao kwa moyo mmoja, wakisema, Mola, wewe ndiwe Mungu, ndiwe uliyefanya mbingu na nchi na bahari na vitu vyote vilivyomo; nawe ulinena kwa Roho Mtakatifu kwa kinywa cha babaetu Daudi, mtumishi wako, Mbona mataifa wamefanya ghasia, Na makabila wametafakari ubatili? Wafalme wa dunia wamejipanga, Na wakuu wamefanya shauri pamoja Juu ya Bwana na juu ya Kristo wake. Maana ni kweli, Herode na Pontio Pilato pamoja na Mataifa na watu wa Israeli, walikusanyika katika mji huu juu ya Mtumishi wako mtakatifu Yesu, uliyemtia mafuta, ili wafanye yote ambayo mkono wako na mashauri yako yamekusudia tangu zamani yatokee. Basi sasa, Bwana, yaangalie matisho yao; ukawajalie watumwa wako kunena neno lako kwa ujasiri wote, ukinyosha mkono wako kuponya; ishara na maajabu vifanyike kwa jina la Mtumishi wako mtakatifu Yesu. Hata walipokwisha kumwomba Mungu, mahali pale walipokusanyika pakatikiswa, wote wakajaa Roho Mtakatifu, wakanena neno la Mungu kwa ujasiri.”

Kwa hiyo kwa kuwaombea watumishi wa Mungu kanisa linashiriki kuwatia moyo kiroho kwaajili ya huduma zao, kutunza hisia zao, kuwaombea waweze kuwa na afya njema  na waweze kustahimili hasa wanapokutana na upinzani, waweze kubeba vema majukumu ya kikanisa na wawe na nguvu wakati wa kupambana na vita vya kiroho, kufanya hivyo pia ni njia ya kushiriki Baraka ya kazi wanayoifanya ya kuihubiri injili kwa usahihi na kuwalinda dhidi ya yule muovu, Mungu awape hekima ya maongozi, lakini zaidi ya yote ni njia ya kuonyesha upendo na ushirika pamoja nao.

Maandiko yanaonyesha pia shetani anaweza kuwazuia watumishi wa Mungu wasilifikie eneo Fulani kwa injili, Anga la Thesalonike lilikuwa gumu kwa Paulo mtume alipohubiri Thesalonike alikutana na upinzani mkali sana lakini sio hivyo tu hata alipotaka kurejea tena kwa kusudi la kuwaimarisha Shetani alimzuia na watumishi wengine, kwa hiyo shetani ni adui wa injili na ni adui wa wale wanaoipeleka injili anaweza kuwazuia wasifike eneo Fulani

1Wathesalonike 2:17-18 “Lakini sisi, ndugu, tukiwa tumefarakana nanyi kwa kitambo, kwa uso si kwa moyo, tulizidi kutamani kwa shauku nyingi kuwaona nyuso zenu.Kwa hiyo tulitaka kuja kwenu, naam, mimi Paulo, mara ya kwanza, na mara ya pili, na Shetani akatuzuia.”

Kama shetani anaweza kumzuia Paulo Mtume na timu yake wasifike Thesalonike kuwaimarisha wakristo waliozaliwa katika hali ya dhiki nyingi tena sio mara moja jiulize anashindwaje kutuzuia wewe na mimi ambao hatuna mwombezi zaidi ya wake zetu, tena wakati mwingine anatugonganisha nao ili maombi yetu yazuiliwe, tunahitaji maombi ya watu waaminifu atakaotambua kile ambacho tumekibeba na kulia na kuomboleza na kufunga kwaajili yetu. 

Hatimaye ndugu tuombeeni

2Wathesalonike 3:1-4 “Hatimaye, ndugu, tuombeeni, neno la Bwana liendelee, na kutukuzwa vile vile kama ilivyo kwenu; tukaokolewe na watu wasio haki, wabaya; maana si wote walio na imani. Lakini Bwana ni mwaminifu, atakayewafanya imara na kuwalinda na yule mwovu. Nasi tumemtumaini Bwana kwa mambo yenu, kwamba mnayafanya tulivyowaagiza, tena kwamba mtayafanya.”

Wote tunafahamu kuwa Paulo Mtume alikuwa ni moja ya viongozi hodari sana katika kuifanya kazi ya Mungu, Neno la Mungu linaonyesha ya kuwa Paulo mtume alitumiwa na Mungu kwa viwango vikubwa na vya juu sana katika kulijenga kanisa la Mungu, naweza kusema kuwa hakuna mtu anaweza kudai kuwa yeye ni wa kiroho kumzidi Paulo Mtume neno la Mungu linaonyesha ya kuwa alifanya kazi kuliko mitume wote, alipewa mafunuo makubwa kuliko mtu yeyote, lakini pia alitumiwa na Mungu kufanya miujiza ya kupita kawaida kwa mikono yake

1Wakorintho 15:9-10 “Maana mimi ni mdogo katika mitume, nisiyestahili kuitwa mitume, kwa sababu naliliudhi Kanisa la Mungu. Lakini kwa neema ya Mungu nimekuwa hivi nilivyo; na neema yake iliyo kwangu ilikuwa si bure, bali nalizidi sana kufanya kazi kupita wao wote; wala si mimi, bali ni neema ya Mungu pamoja nami.”

2Wakorintho 12:2-4 “Namjua mtu mmoja katika Kristo, yapata sasa miaka kumi na minne, (kwamba alikuwa katika mwili sijui; kwamba alikuwa nje ya mwili sijui; Mungu ajua). Mtu huyo alinyakuliwa juu mpaka mbingu ya tatu. Nami namjua mtu huyo, (kwamba alikuwa katika mwili sijui; kwamba alikuwa nje ya mwili sijui; Mungu ajua); ya kuwa alinyakuliwa mpaka Peponi, akasikia maneno yasiyotamkika, ambayo haijuzu mwanadamu ayanene.”

Matendo 19:11-12 “Mungu akafanya kwa mikono ya Paulo miujiza ya kupita kawaida; hata wagonjwa wakaletewa leso na nguo zilizotoka mwilini mwake, magonjwa yao yakawaondokea, pepo wachafu wakawatoka.”

Hata pamoja na kutumiwa hivyo sana na Mungu, na kupewa mafunuo makubwa sana na kufanya kazi ya Mungu kwa neema kubwa kuliko mitume wote bado Paulo mtume kwa unyenyekevu mkubwa alionekana katika nyaraka nyingi akiomba kuombewa, mara kwa mara utaona akiomba maombi, ndugu tuombeeni, hatimaye ndugu tuombeeni, jitahidini pamoja nami katika maombi, hakuwa na kiburi wala hakufikiri kuwa anaweza peke yake na kumbuka kuwa yeye mwenyewe alikuwa mwombaji, watu wengi sana wa Mungu hawaijui siri hii wanadhani kuomba kuombewa na washirika ni kuonyesha  udhaifu, wanadhani ni sisi tu ndio wenye wajibu wa kuwaombea washirika  na ni kama washirika hawapaswi kutuombea  jambo hilo sio sahihi, au kuwa na timu ya watu wanaoomba kwaajili yako au hata wanaoomba pamoja nawe, huo sio udhaifu ni unyenyekevu na ni ukweli usiopingika kibiblia kuwa tunahitaji kuombewa, tunahitaji watu waaminifu, waliojitoa wanaojua nini wanakifanya kutuombea, tunahitaji maombi!

Warumi 15:30-32 “Ndugu zangu, nawasihi kwa Bwana wetu Yesu Kristo, na kwa upendo wa Roho, jitahidini pamoja nami katika maombi yenu kwa ajili yangu mbele za Mungu; kwamba niokolewe na wale wasioamini katika Uyahudi, na tena huduma yangu niliyo nayo huko Yerusalemu ikubalike kwa watakatifu; nipate kufika kwenu kwa furaha, kama apendavyo Mungu, nikapate kupumzika pamoja nanyi.”

Waefeso 6:18-20 “kwa sala zote na maombi mkisali kila wakati katika Roho, mkikesha kwa jambo hilo na kudumu katika kuwaombea watakatifu wote; pia na kwa ajili yangu mimi, nipewe usemi kwa kufumbua kinywa changu, ili niihubiri kwa ujasiri ile siri ya Injili; ambayo kwa ajili yake mimi ni mjumbe katika minyororo; hata nipate ujasiri katika huyo kunena jinsi inipasavyo kunena.”

Wakolosai 4:2-3 “Dumuni sana katika kuomba, mkikesha katika kuomba huku na shukrani; mkituombea na sisi pia, kwamba Mungu atufungulie mlango kwa lile neno lake, tuinene siri ya Kristo, ambayo kwa ajili yake nimefungwa,”

2Wakorintho 1:9-11. “Naam, sisi wenyewe tulikuwa na hukumu ya mauti katika nafsi zetu ili tusijitumainie nafsi zetu, bali tumtumaini Mungu, awafufuaye wafu, aliyetuokoa sisi katika mauti kuu namna ile; tena atatuokoa; ambaye tumemtumaini kwamba atazidi kutuokoa; ninyi nanyi mkisaidiana nasi kwa ajili yetu katika kuomba, ili, kwa sababu ya ile karama tupewayo sisi kwa msaada wa watu wengi, watu wengi watoe shukrani kwa ajili yetu.”

Tunapowaombea watumishi wa Mungu wanapewa ujasiri, wanatumiwa na Mungu kwa miujiza, neno la Mungu linaenea kwa nguvu huku likishinda nguvu za upinzani, milango ya injili inafunguka, wananusuriwa na hatari za namna mbalimbali, huduma inaenea katika mataifa mengi kama wana kesi au wamefungwa minyororo inaachilia, lakini zaidi ya yote wanalindwa ili kwamba wasipepetwe katika imani wala imani zao zisitindike, Yesu alimuombea Petro awe imara,  Imani yake isitindike, ni maombi  yet utu ndio yatakayowadumisha watumishi wa Mungu na kuwafanya imara katika imani, mtumishi asiyeombewa hawezi kusimama, washirika wasio na akili husengenya na kuwashutumu watumishi wa Mungu wanapoingia majaribuni wakisahau kuwa hawajawahi hata siku moja kufanya wajibu wao wa kumlilia Mungu kwaajili yao ili wasimame imara na kushinda vikwazo vyote vinavyowakabili.

Luka 22:31-32. “Akasema, Simoni, Simoni, tazama, Shetani amewataka ninyi apate kuwapepeta kama vile ngano; lakini nimekuombea wewe ili imani yako isitindike; nawe utakapoongoka waimarishe ndugu zako.”

Mifano ya watumishi wa Mungu waliokuwa na timu za waombaji

Kwa kufahamu siri hii ya kuwa kila mtumishi wa Mungu anahitaji maombi, baadhi ya watumishi wa Mungu waligundua kuwa kama Paulo Mtume aliyekuwa wa kiroho sana bado kuna nyakati alihitaji maombi ni zaidi sana mimi na wewe tunahitaji maombi, ndugu unahitaji kuombewa ninahitaji sana maombi yako pia, Katika historia ya kanisa, wahubiri wengi waliotumiwa na Mungu na kuleta uamsho mkubwa hawakuwa wanategemea kipawa na upako wao peke yao,  wala maombi yao peke yao lakini vile vile walikuwa na timu maalumu za waombaji waliobeba huduma zao kwa maombi endelevu na ya kudumu!

John Wesley – alizaliwa june 28 1703 na kufariki 2March 1791 moja ya mwinjilisti mkubwa sana duniani na mwanatheolojia maarufu ambaye likuwa sababu ya uamsho mkubwa wa kanisa la Uingereza, alikuwa na vikundi vidogo vidogo vingi kama madarasa ya maombi, hakuruhusu kufanya huduma bila nidhamu ya kiroho, alisababisha uamsho mkubwa huko uingereza na kusababisha mabadiliko makubwa ya kijamii, maadili  katika kazi na familia  na kusababisha kanisa lililodumu hadi leo, tunajifunza kwake kuwa maombi ya pamoja huzalisha mabadiliko ya kitaifa

Charles Finney – Ni moja ya wahubiri waliotumiwa sana na Mungu kuleta uamsho mkubwa alizaliwa 29 August 1792 na kufariki mwaka 16 August 1875, alikuwa ni muhudumu wa kanisa la American Presbyterian alijulikana  sana kama kiongozi wa uamsho mkubwa wa Pili katika Marekani, alikuwa akisimama kabla hata ya kuhubiri watu walililia toba kabla ya mahubiri kuanza na kulikuwa na uamsho mkubwa sana nyakati zake lakini yeye alisema wazi “Mahubiri yangu yalibebwa na Maombi ya Nash” Daniel Nash maarufu kama (Father Nash) alikuwa mtu mmoja maalumu ambaye kazi yake ilikuwa ni kuomba bila kukoma kabla ya Finney kuhubiri, Daniel Nash alikuwa anaenda katika mji husika ambao Finney angehubiri kwa muda kuanzia wiki au miezi kabla, akifunga na kuomba, Mahubiri yenye matokeo makubwa sana hutanguliwa na maombi makubwa sana.

D. L Moody – Moja ya wainjilisti maarufu sana Duniani  alizaliwa February 5 1837 na kufariki December 1899 jina lake kwa urefu ni Dwight Lyman Moody maarufu kama D.L Moody mwinjilisti maarufu wa kimarekani alihubiri injili na kusababisha maelefu ya watu kuokoka huko ulaya na Marekani, aliendelea na huduma bila kuwa na Skendo injili ilienea kupitia yeye kizazi kwa kizazi  lakini yeye alikuwa na timu ya waombaji waliokuwa wakikaa nyuma ya pazia wakati yeye alipokuwa anahubiri alisema “Ni Afadhali nopate watu 10 wanaoomba kuliko 10,000 wanaonisikiliza” mafanikio yoyote ya jukwaani ni matokeo ya kazi katika chumba cha maombi

Reinhard Bonnke – Muhubiri mkubwa sana Duniani chini ya huduma ya Christ for All nations (CfaN) amehubriri watu zaidi ya milioni 79 waliookoka katika huduma yake, Mungu alimtumia kwa miujiza mikubwa wakati akihubiri Afrika, huduma yake ilimuwezesha kutembelea bara zima, Muhubiri huyu mwenye asili ya Ujerumani alikuwa na mtandao mkubwa sana wa kimataifa wa waombaji, ambao walifunga wiki kadhaa na saa kadhaa kila alipokuwa akifanya mkutano wa injili Bonke alikuwa na timu mahususi ya kuombea huduma yake kwa hiyo tunajifunza hapo kuwa Huduma kubwa huitaji Jeshi kubwa la siri la waombaji.

Billy Graham – Moja ya wahubiri wakubwa walioheshimika sana Marekani alizaliwa 7 November 1918 na kufariki 21 February 2018 alikuwa na timu ya maombi iliyoitwa “The prayer Partners” yeye hakuwahi kukubali mkutano wowote ufanyike bila maandalizi ya maombi ya muda mrefu, Mungu alimpa neema ya kuhubiria maraisi wa aina mbalimbali, mataifa mengi na mamilioni ya watu alikaa katika huduma kwa karibu miaka 60 bila kuharibiwa na maswala ya fedha, umaarufu kiburi au wanawake, tunajifunza kutoka kwake ya kuwa maombi hutunza sio huduma tu hata sifa nzuri za muhubiri anayeombewa.

David Yonggi Cho – Mwanzilishi wa Kanisa la Yoido Full Gosple Church alizaliwa 14 February 1936 na kufariki 14 september 2021 ni moja ya waanzilishi wa maswala ya mlima wa maombi (Prayer Mountain) alitenga wachungaji na waombaji kila wakati kwaajili ya kufunga na kuomba na kukemea au kupigana vita vya kiroho, matokeo yake akawa ndiye mchungaji mwenye kanisa kubwa zaidi kuliko watu wote duniani kwa nyakati zake, alichangia kwa kiasi kikubwa uamsho ulioko Korea ya kusini, na alifanikiwa kwa kuanzisha mfumo wa cell groups au makanisa ya nyumbani ambao nao ulibebwa na maombi, tunajifunza kutoka kwake kuwa kanisa linalotaka kukua kwa haraka lazima lijikite katika mzizi wa kuomba.

Zachary Kakobe – Ni mwanzilishi wa Kanisa la Full Gospel Bible Fellowship nchini Tanzania, moja ya makanisa ya kipentekoste yenye asili yake nchini Tanzania na si kutoka nje, Muhubiri maarufu sana mwenye kanisa kubwa huko Mwenge jijini Dar es Salaam, Mchungaji Kakobe ana mfumo wa cell ziitwazo “Power House” ambapo washirika katika maeneo mbalimbali kila mtaa waliko washirika hukutana kila alhamisi kwa maombi mbalimbali  ya kikanisa ikiwa ni pamoja na kumuombea Mchungaji, aidha ana kikundi maalumu ya maombi kijulikanacho kwa jina la  Ana binti Fanuel ambao pamoja na mambo mengine humuombea Mchungaji sawasawa na maelekezo yake kikundi hiki kinaundwa na wajane maalumu ambao hutunzwa na kanisa, Matokeo yake Kanisa lake limeweza kuenea nchi nzima kwa muda mfupi, kuna uamsho mkubwa sana unaofukuta chini kwa chini, washirikia wake wamejengwa katika misingi ya kuomba kwa kuyataja maandiko, wanapenda mafundisho na wanaishi kwa nidhamu. Alizaliwa 6 June 1955 huko, Kakonko, Kigoma, uamsho katika kanisa lake unakua kwa kasi kupitia maombezi, semina na mikutano ya ndani kwa ndani, pamoja na yeye mwenyewe kuwa mwombaji, Kakobe mara kwa mara amesisitiza kuombewa, kama ilivyokuwa kwa Paulo mtume, Kumbe maombi yana nguvu ya kuwaleta maelefu kwa Yesu, kuwafanya wanafunzi hata bila kuathiri, shughuli na utendaji wa maisha ya kawaida ya watu na kujenga kanisa imara

 

Hitimisho!

Unapochunguza kwa makini mifano hii michache ya wahubiri ambao Mungu aliwatumia kwa uamsho mkubwa sehemu mbalimbali duniani utabaini kuwa maombi yanahusika kwa kiasi kikubwa, sitaki kusema kuwa kila uamsho unaletwa na maombi lakini nataka kusema kuwa, mahuburi na uamsho wa kina na endelevu unajengwa kwa maombi, watumishi wa Mungu tutake maombi kwa washirika wetu, hata pamoja na sisi wenyewe kuwa waombaji, lakini pia tuwe na timu za maombi watu wanaotuombea kwa kina, na sio vibaya kuwa na timu ya watu wanaoomba pamoja nawe au wanaokuombea, Yesu alimtaka Petro, Yakobo na Yohana, wakeshe au waombe pamoja naye, Licha ya kuwa alikuwa wa kiroho sana na ni mwana wa Mungu, nadhani ni afadhali mara elfu kuwa na waombaji  wanaokuombea kwa huduma yako kuliko kuwa na walinzi wanaokulinda “Body guards

Mathayo 26:36-38 “Kisha Yesu akaenda pamoja nao mpaka bustani iitwayo Gethsemane, akawaambia wanafunzi wake, Ketini hapa, hata niende kule nikaombe. Akamchukua Petro na wale wana wawili wa Zebedayo, akaanza kuhuzunika na kusononeka.Ndipo akawaambia, Roho yangu ina huzuni nyingi kiasi cha kufa; kaeni hapa, mkeshe pamoja nami.”

Mtumishi wa Mungu mwombe Mungu akupe watu sahihi watakaokubebea mzigo katika maombi, omba Mungu akupe hekima kuchagua watu wasiri waliojaa maisha ya maombi wanyenyekevu, waaminifu, wenye upendo na mzigo au wajane wenye umri mkubwa wanaofanya kazi ya kuomboleza kwaajili yako, waelezee maono yako au mzigo unaotaka wakubebee, wafundishe masomo mbalimbali kuhusu kuomba, tengeneza mfumo au muda maalumu wa kuomba na siku maalumu za kuomba,  hata pamoja na kuwa na idara za maombi, amini sana katika watu wachache ambao maalumu au kipekee watakuwa wanakuombea, anza na watu wachache sana kikundi cha maombi kinatakiwa kuwa na watu 3-12 tengenezeni mawasiliano ya siri, wafundishwe kuishi maisha ya kujitoa na utakatifu, wenye matumizi mazuri ya kinywa wasio na mafarakano waandae kwa mafundisho maalumu ya waombaji kwaajili ya mtumishi wa Mungu kisha anzeni kuomba!

 

Na Rev. Innocent Samuel Kamote

Mkuu wa wajenzi mwenye Hekima

Jumapili, 18 Januari 2026

Walinichukia bure!


Zaburi 69:4 “Wanaonichukia bure ni wengi Kuliko nywele za kichwa changu. Watakao kunikatilia mbali wamekuwa hodari, Adui zangu kwa sababu isiyo kweli. Hata mimi nalilipishwa kwa nguvu Vitu nisivyovichukua.”

Yohana 15:24-25 “Kama nisingalitenda kwao kazi asizozitenda mtu mwingine, wasingalikuwa na dhambi; lakini sasa wametuona mimi na Baba yangu, na kutuchukia. Lakini litimie lile neno lililoandikwa katika torati yao, Walinichukia bure.”



Utangulizi:

Je umewahi kupitia hali katika maisha ambapo umekumbana na watu katika mazingira fulani kisha wakakuchukia tu bila ya sababu?  Au wakakupinga tu au wakakukataa, au ukakaliwa vikao, au kuitwa kwenye mabaraza ya watu waliojaa chuki na wivu wewe ukawa ndio agenda na kisha yakatolewa maamuzi ya kukuhukumu wewe hata bila ya sababu yenye mashiko? “Walinichukia bure bila ya sababu” ni moja ya usemi wenye nguvu sana wa kibiblia  ambao kivuli chake ni Zaburi 69:4 na Asili yake ni Yohana 15:24-25 ambapo Daudi pamoja na Yesu Kristo wanaelezea namna na jinsi walivyochukiwa na watu au maadui zao bila ya sababu, wakiwashambulia na kuwachukia  na kuwahukumu, na kuwapinga, na kuwafukuza bila sababu za haki, au kwa sababu ya chuki, wivu na kutokueleweka!, hata ingawa kuchukiwa, kukataliwa, kutokueleweka, na kuhukumiwa isivyo haki kunaweza kuwa na maumivu fulani kisaikolojia au kimwili, lakini kimaandiko jambo hili sio jipya kwani Biblia inatufundisha namna ya kuonyesha jinsi kupokea na kuonyesha mwitikio kwa mambo madogo kama haya kiroho  na sababu kwa nini unachukiwa bure bila sababu za maana, tutajifunza somo hili zuri Walinichukia bure! kwa kuzingatia vipengele vikuu muhimu vitatu vifuatavyo;-

·         Maana ya kuchukiwa bure!

·         Sababu za kuchukiwa bure

·         Jinsi ya kupokea na kuitikia chuki zao za bure


Maana ya kuchukiwa bure!

Yohana 15:24-25 “Kama nisingalitenda kwao kazi asizozitenda mtu mwingine, wasingalikuwa na dhambi; lakini sasa wametuona mimi na Baba yangu, na kutuchukia. Lakini litimie lile neno lililoandikwa katika torati yao, Walinichukia bure.”

Ni muhimu kufahamu kuwa neno kuchukiwa katika lugha ya Kiebrania linatumika neno śānē  ambalo maana yake kwa kiingereza ni to detest, oppose or treat as an enemy  kwa Kiyunani (Greek) ni miseō ambalo kwa kiingereza ni to detest, reject, persecute or love less intentionally  katika msamiati wa kisaikolojia linatumika neno “antipathy” ambalo kiingereza ni a strong feeling of dislike kwa hiyo kuchukiwa katika lugha ya Kiswahili kwa maana hizo hapo juu tunaweza kutafasiri kama Hisia kali za kutokukubali, hisia za kukukataa, hisia za kukupinga, hisia za kukuona kama adui, hisia za kutokukupenda, hisia za kutamani wakutese au upatwe na mabaya au usiwepo, au kuhisi kukuchukia tu bila sababu za maana za makusudi au za kutokukusudia chuki hii inasukumwa na wivu wa kiroho moyoni mwa watu kwa sababu ya kibali cha kiungu ndani yako, kwa hiyo chuki hii wakati mwingine inaweza kutoka kwa watu waliokuzidi kila kitu,  wana cheo, wana mali, wana elimu, wakati mwingine hata umri mkubwa kuliko wako lakini wakikuona tu wanakuchukia bila sababu na unaweza kujiuliza mbona mimi sina lolote kama wao lakini wanakuchukia tu, Daudi anasema walionichukia ni hodari  wanaotamani kumkatilia mbali wana nguvu lakini hata hivyo walimchukia bure tu, hii ni chuki ambayo asili yake ni mambo ya rohoni na wivu wenye uchungu!

Zaburi 69:4 “Wanaonichukia bure ni wengi Kuliko nywele za kichwa changu. Watakao kunikatilia mbali wamekuwa hodari, Adui zangu kwa sababu isiyo kweli. Hata mimi nalilipishwa kwa nguvu Vitu nisivyovichukua.”

Hapo tumeona maana ya neno chuki lakini vile vile neno “bure” katika biblia ya kiebrania linasomeka kama “hinnām” ambalo kwa kiingereza ni “unjustly” na katika biblia ya kiyunani linasomeka kama “dōrean” ambalo maana yake “undeservedly”  katika Kiswahili cha kimahakama kuchukiwa huku kulikuwa kusikokuwa na sababu za haki, kwa dhuluma, bila makosa ya kimahakama, bila kukutwa na hatia, isivyohalali, kwa hiyo watu wanaweza kukuchukia wewe kwa sababu isiyoweza kuthibitishwa kimahakama, kwamba mtuhumiwa ana makosa gani, kwa mfano Daudi alilipishwa kwa nguvu vitu ambavyo hakuvichukua, au Yesu alihukumiwa mahakamani huku hakimu akigundua kuwa ilikuwa ni wivu tu, walimtoa kwa husuda, hakuwa amewakosea wao, wala mtu yeyote.

Mathayo 27:17-18 “Basi walipokutanika, Pilato akawaambia, Mnataka niwafungulie yupi? Yule Baraba, au Yesu aitwaye Kristo? Kwa maana alijua ya kuwa wamemtoa kwa husuda.”

Unaona ndugu yangu unaweza kuchukiwa bure katika maisha haya ya kutembea na Yesu unaweza kupigwa vita, unaweza kuchukiwa bila ya sababu, unaweza kuchukiwa kwa sababu zisizo za kweli wala za haki, unaweza kuchukiwa hata na watu uliowahi kuwaomba msamaha hata pamoja na kuwa wamekukosea wao, chuki hii ni chuki ya husuda na haina mashiko, yanapokutokea haya katika maisha ya wokovu na wakati mwingine kutoka kwa watu waliookoka tena wenye nguvu kuliko wewe fahamu umebeba kusudi kubwa na maalumu, fahamu wewe ni mwanafunzi wa Yesu kweli kweli wala usifadhaike, Neno la Mungu linatufunulia siri hizo muhimu zinazopelekea wewe uchukiwe

Sababu za kuchukiwa bure.

Ni muhimu kufahamu kuwa chuki za bure kwako zinafunua maana pana sana za kiwango cha kiroho ulichokifikia, wakristo wengi leo wanaishi maisha ya kinafiki na sio wakweli kwa Mungu wala kwa wanadamu, wengi wanaishi maisha ya kuigiza, wanaonekana kama watu maarufu kwa nje, wakiwa na elimu kubwa, na vyeo vikubwa na wenye pesa na nguvu lakini hawana nguvu za kiroho walishakufa zamani na wamepoteza kabisa kujiamini, na kiroho wamefilisika, unapokuwa mwanafunzi wa kweli wa Yesu na mfuasi wa kweli wa Bwana Yesu katika karne hizi, watakupendea nini? Wakupende kwa lipi? Kama wewe ni mwana wa Mungu tu hawakupendi, kama hujawahi kuwafanya lolote tu wanakuchukia bure je wataweza kuwapenda adui wa kweli ambao Yesu amesema wapendeni adui zenu? Waombeeni wanaowaudhi?, huoni kuwa agizo hilo ni la juu zaidi? Wewe maisha yako yanawapa tabu, kama Yesu alivyowapa taabu mafarisayo na masadukayo, kwa hiyo unapoona wanakuchukia bure ziko sababu nyingi na hapa na ainanisha chache:-

1.       Kwa sababu wewe ni nuru – Mtu wa Mungu ni hivi unapoishi maisha ya nuruni, hapa maana yake wewe ni mkweli kwa Mungu, unapokosea unatubu, na unasonga mbele na huna kinyongo na mtu na Mungu yuko upande wako na anakutetea na kukupigania basi elewa hivi maisha yako ya nuruni yanalifanya giza lidhalilike, hata kama husemi lolote lakini kuishi kwako kwa haki hata bila ya maneno kunawafunua wenye dhambi, kwa hiyo watu wanaweza kukuchukia sio kwa sababu ya kitu umefanya bali kwa sababu kuna kitu unakiwakilisha

 

Yohana 3:19-21 “Na hii ndiyo hukumu; ya kuwa nuru imekuja ulimwenguni, na watu wakapenda giza kuliko nuru; kwa maana matendo yao yalikuwa maovu. Maana kila mtu atendaye mabaya huichukia nuru, wala haji kwenye nuru, matendo yake yasije yakakemewa. Bali yeye aitendaye kweli huja kwenye nuru, ili matendo yake yaonekane wazi ya kuwa yametendwa katika Mungu.”

 

1Yohana 2:9-11 “Yeye asemaye kwamba yumo nuruni, naye amchukia ndugu yake, yumo gizani hata sasa. Yeye ampendaye ndugu yake, akaa katika nuru, wala ndani yake hamna kikwazo. Bali yeye amchukiaye ndugu yake, yu katika giza, tena anakwenda katika giza, wala hajui aendako, kwa sababu giza imempofusha macho.”          

 

2.       Kwa sababu wewe si wa ulimwengu huu – Mtu wa Mungu kama wewe ni wa Yesu Kristo hivi unadhani ulimwengu utakupenda? Ukupende wewe nani? Ukupende wewe umeutendea nini? Ukupende wakati unafunua siri za Mungu? Ukupende wakati hata Yesu Mwenyewe walimchukia bure wewe kama u mwanafunzi wa Yesu utachukiwa tu, Yesu alisema kama mimi mwenyewe walinickukia mwanafunzi hampiti Mwalimu wake yaani kila mwanafunzi wa kweli wa Yesu atachukiwa tu, mpendwa chuki hiyo ni ushahidi wa wazi kwamba unamlingania Yesu Kristo, kuchukiwa kwako sio ushahidi wa kushindwa kwako bali ni ushahidi ya kuwa unamuishia Yesu Kristo  na sio hivyo tu hata mafundisho yetu yatakataliwa kama yalivyokataliwa ya Yesu

 

Yohana 15:18-20 “Iwapo ulimwengu ukiwachukia, mwajua ya kuwa umenichukia mimi kabla ya kuwachukia ninyi. Kama mngekuwa wa ulimwengu, ulimwengu ungewapenda walio wake; lakini kwa kuwa ninyi si wa ulimwengu, bali mimi naliwachagua katika ulimwengu, kwa sababu hiyo ulimwengu huwachukia. Likumbukeni lile neno nililowaambia, Mtumwa si mkubwa kuliko bwana wake. Ikiwa waliniudhi mimi, watawaudhi ninyi; ikiwa walilishika neno langu watalishika na lenu.”

 

3.       Kwa sababu wewe ni wa rohoni na wao ni wa mwilini – Mtu wa Mungu ninataka nikuambie ya kwamba ulimwengu tulio nao una makundi makuu mawili tu, haijalishi kundi hilo liko kanisani au nje lakini kokote kwenye watu kuna aina mbili za watu watu wa rohoni na watu wa mwilini, wale wa mwilini huwaudhi wale wa rohoni hii ni kanuni ya kibiblia iliyokuwako zamani na inatenda kazi hata sasa, kama wewe ni mzaliwa wa kiroho utaudhiwa na yule wa mwilini tu ona  

 

Wagalatia 4:29 “Lakini kama vile siku zile yule aliyezaliwa kwa mwili alivyomwudhi yule aliyezaliwa kwa Roho, ndivyo ilivyo na sasa.”

 

4.       Kwa sababu ya kibali cha Mungu juu yako – Ndugu yangu mpendwa kama Mungu amekupa kibali, Mungu amekupaka mafuta, Mungu ana matumizi na wewe Mungu ana kusudi na wewe kibali cha Mungu juu yako kinawanyanyasa kisaikolojia wale wasio na kibali hicho sasa wakuchekee? Wakutie moyo, wakukubali wakati wanatamani kusikia umeharibikiwa, wanatamani hata ufe leo, Daudi anasema wanaomchukia ni wengi kuliko nywele za kichwa chake, kaangalie mashariki ya kati Israel inapendwa? Wanatamani waifutilie mbali wanatamani waikatilie mbali ndivyo ulivyo na wewe mtu wa Mungu, kibali chako kinawasumbua haijalishi hali ya nje kuwa wao wana nguvu lakini upako wako unawanyanyasa ndio maana wanakuchukia bure

 

1Samuel 29:6-8 “Hata ikawa, walipokuwa wakienda, hapo Daudi aliporudi baada ya kumwua yule Mfilisti, wanawake wakatoka katika miji yote ya Israeli, kwa kuimba na kucheza, ili kumlaki mfalme Sauli; wakatoka na matari, na shangwe, na vinanda. Nao wale wanawake wakaitikiana wakicheza, wakasema, Sauli amewaua elfu zake, Na Daudi makumi elfu yake. Basi Sauli akaghadhibika sana, na maneno haya yakamchukiza; akasema, Wamempa Daudi makumi elfu, na mimi wamenipa elfu tu; kuna nini tena awezayo kupata, isipokuwa ni ufalme?

 

Mwanzo 37:3-11 “Basi Israeli akampenda Yusufu kuliko wanawe wote, maana ni mwana wa uzee wake, akamfanyia kanzu ndefu. Ndugu zake wakaona ya kuwa baba yao anampenda kuliko ndugu zake wote, wakamchukia, wala hawakuweza kusema naye kwa amani. Yusufu akaota ndoto, akawapa ndugu zake habari, nao wakazidi kumchukia; akawaambia, Tafadhalini, sikieni ndoto hii niliyoiota. Tazama, sisi tulikuwa tukifunga miganda shambani, kumbe! Mganda wangu ukaondoka ukasimama, na tazama, miganda yenu ikazunguka ikainama mbele ya mganda wangu. Ndugu zake wakamwambia, Je! Kweli wewe utatumiliki sisi? Nawe utatutawala sisi? Wakazidi kumchukia kwa ajili ya ndoto yake, na kwa maneno yake. Akaota tena ndoto nyingine, akawaambia ndugu zake, akasema, Angalieni, nimeota ndoto nyingine; na tazama, jua na mwezi na nyota kumi na moja zikaniinamia. Akawaambia baba yake na ndugu zake; baba yake akamkemea akamwambia, Ni ndoto gani hii uliyoiota? Je! Mimi na mama yako na ndugu zako tutakuja tukusujudie hata nchi? Ndugu zake wakamhusudu; bali baba yake akalihifadhi neno hili.”

 

5.       Kwa sababu ya wivu wenye uchungu – Mpendwa wakati mwingine wewe unachukiwa bure kwa sababu ya wivu, ni wivu tu, kuna kitu wakijilinganisha na wewe au na ninyi  wanakuona kabisa unakwenda mbele, wanakuona kabisa uko tofauti hata kama kwa sasa huna kitu wanakuona na wanajua uweza wa Mungu juu yako na kile ambacho Mungu amewekeza ndani yako wakupende kwa lipi wakati wamejaa wivu, wamejaa wivu huu ni wivu wenye uchungu wivu wa kujilinganisha na wao na wakijilinganisha na wewe wanaona kuna kitu cha ziada kwako wivu huu wa kujilinganisha unaitwa “phthonos” kwa kiingereza “is hatred rooted in comparison”  Yesu alichukiwa kwa sababu alikuwa na kitu cha ziada kuliko mafarisayo na masadukayo, kwa hiyo walikuwa na wivu uliojaa chuki aina hii ya wivu wakati mwingine huwazungumzia watu vibaya  na mambo mabaya ili wao waonekane wema yule mwema aonekane mbaya.

 

Mathayo 27:17-18 “Basi walipokutanika, Pilato akawaambia, Mnataka niwafungulie yupi? Yule Baraba, au Yesu aitwaye Kristo? Kwa maana alijua ya kuwa wamemtoa kwa husuda.”

 

Matendo 5:16-20 “Nayo makutano ya watu wa miji iliyoko kandokando ya Yerusalemu wakakutanika, wakileta wagonjwa, nao walioudhiwa na pepo wachafu; nao wote wakaponywa. Akaondoka Kuhani Mkuu na wote waliokuwa pamoja naye, (hao ndio walio wa madhehebu ya Masadukayo), wamejaa wivu, wakawakamata mitume wakawaweka ndani ya gereza; lakini malaika wa Bwana akafungua milango ya gereza usiku, akawatoa, akasema, Enendeni mkasimame hekaluni mkawaambie watu maneno yote ya Uzima huu.”

 

Waebrania 12:14-15. “Tafuteni kwa bidii kuwa na amani na watu wote, na huo utakatifu, ambao hapana mtu atakayemwona Bwana asipokuwa nao; mkiangalia sana mtu asiipungukie neema ya Mungu; shina la uchungu lisije likachipuka na kuwasumbua, na watu wengi wakatiwa unajisi kwa hilo.”    

 

6.       Kwa sababu ya vita vya kiroho – Wakati mwingine ile chuki inatokana na mapepo, kwa kadiri shetani alivyo adui yetu na anavyotuchukia sisi ndivyo anavyowatumia mapepo na maajenti wake au wakristo dhaifu kutumiwa na mapepo kutushambulia kwa hio wakati mwingine hii chuki kubwa unayoiona dhidi yako mtu wa Mungu ni ya shetani akiwatumia watu wake au vyombo vyake ili kupingana na kile ambacho Mungu amewekeza ndani yako

 

Waefeso 6:12 “Kwa maana kushindana kwetu sisi si juu ya damu na nyama; bali ni juu ya falme na mamlaka, juu ya wakuu wa giza hili, juu ya majeshi ya pepo wabaya katika ulimwengu wa roho.”

 

7.       Kwa sababu ya kuishi maisha ya utauwa -  kila unapokusudia na kuthubutu kuishi maisha ya tofauti na wengine maisha ya utakatifu na kuimarisha uhusiano wako wa siri na Mungu watu wabaya  na wadanganyaji wanaendelea kuteseka  na watakucukia, wewe jaribu kuishi na kuigiza kila alichikifanya bwana Yesu, jitoe kama yeye fuata mfano wake uone kama dunia itakupongeza hata kidogo!  Utachukiwa, utateswa, utadhihakiwa, utakataliwa, utaonekana huna faida, kwa sababu maisha ya kujitoa kwa Mungu yanapingana nay a dunia hii, viwango vya kuishi kama Kristo vinawaudhi wahuni,  vinawapa changamoto na kuwafanya wote walio vufuvugu na wasiookoka  wakose Amani, kwa hiyo kuchukiwa ni sehemu ya gharama za uaminifu wako kwa Mungu au kumfuata Yesu kwa uaminifu

 

2Timotheo 3:12-15 “Naam, na wote wapendao kuishi maisha ya utauwa katika Kristo Yesu wataudhiwa. lakini watu wabaya na wadanganyaji wataendelea, na kuzidi kuwa waovu, wakidanganya na kudanganyika. Bali wewe ukae katika mambo yale uliyofundishwa na kuhakikishwa, kwa maana unajua ni akina nani ambao ulijifunza kwao; na ya kuwa tangu utoto umeyajua maandiko matakatifu, ambayo yaweza kukuhekimisha hata upate wokovu kwa imani iliyo katika Kristo Yesu.”   

 

Jinsi ya kupokea na kuitikia chuki zao za bure

Ni jambo la kumshukuru Mungu kwamba Mungu ametupa akili na ufahamu katika neno lake namna na jinsi ya kushughulika na watu wanaotuchukia na njia hizo ni njia za kiroho, ambazo kimsingi zitakufanya wewe kuzidi bali adui zako kupungua, njia hizi ukizitumia zitakamilisha uwezo wako wa kiroho na kukunoa na kukufanya wewe uendelee kukua kiroho zaidi na kumfanania baba wa mbinguni

1.       Kunyamaza kimya – Moja ya njia ya kiroho ambayo Yesu Kristo aliitumia pale waliokuwa wakimchukia walipokuwa wakimsingizia mambo ya uongo ambayo hayana ukweli wowote bali kwa lengo la kumchafua na kuharibu tu wito wake yeye alikaa kimya, alipoonewa aikaa kimya alipoteswa na kutukanwa alikaa kimya, Neno kukaa kimya katika kiyunani ni “loidoreō kwa kiingereza ni “revile” ambalo maana yake ni “to insult verbally” hakutumia lugha chafu kujibu alinyamaza kimya badala ya kujibu “silence over revenge”  na alijikabidhi kwa Mungu ahukumuye kwa haki, Mpendwa mwachie Mungu atajibu kwa haki, Mungu huwapigania watu wakimya

 

1Petro 2:21-23 “Kwa sababu ndio mlioitiwa; maana Kristo naye aliteswa kwa ajili yenu, akawaachia kielelezo, mfuate nyayo zake.Yeye hakutenda dhambi, wala hila haikuonekana kinywani mwake. Yeye alipotukanwa, hakurudisha matukano; alipoteswa, hakuogofya; bali alijikabidhi kwake yeye ahukumuye kwa haki.”

 

Isaya 53:7 “Alionewa, lakini alinyenyekea, Wala hakufunua kinywa chake; Kama mwana-kondoo apelekwaye machinjoni, Na kama vile kondoo anyamazavyo Mbele yao wakatao manyoya yake; Naam, hakufunua kinywa chake.”

 

Hesabu 12:1-9 “Kisha Miriamu na Haruni wakamnenea Musa kwa sababu ya mwanamke Mkushi aliyekuwa amemwoa; maana, alikuwa amemwoa mwanamke Mkushi. Wakasema, Je! Ni kweli Bwana amenena na Musa tu? Hakunena na sisi pia? Bwana akasikia maneno yao. Basi huyo mtu, huyo Musa, alikuwa mpole sana zaidi ya wanadamu wote waliokuwa juu ya uso wa nchi. Bwana akanena ghafula na Musa, na Haruni na Miriamu, na kuwaambia, Tokeni nje ninyi watatu, mwende hemani mwa kukutania. Basi hao watatu wakatoka nje. Bwana akashuka katika nguzo ya wingu akasimama pale mlangoni pa Hema, akawaita Haruni na Miriamu, nao wakatoka nje wote wawili. Kisha akawaambia, Sikizeni basi maneno yangu; Akiwapo nabii kati yenu, Mimi, Bwana, nitajifunua kwake katika maono, Nitasema naye katika ndoto. Sivyo ilivyo kwa mtumishi wangu, Musa; Yeye ni mwaminifu katika nyumba yangu yote; Kwake nitanena mdomo kwa mdomo, Maana, waziwazi wala si kwa mafumbo; Na umbo la Bwana yeye ataliona. Mbona basi ninyi hamkuogopa Kumnenea mtumishi wangu, huyo Musa? Hasira za Bwana zikawaka juu yao; naye akaenda zake.”

 

2.       Waombee wanao kuudhi – Maandiko yanatufundisha kutoka mafundisho na maendo ya Bwana wetu Yesu na watakatifu walioyutangulia kuwa kuna haja ya kuwaombea wale wanaotuchukia, tuwaonee huruma na tuwapende kwa sababu wao ni dhaifu

 

Mathayo 5:43-45 “Mmesikia kwamba imenenwa, Umpende jirani yako, na, Umchukie adui yako; lakini mimi nawaambia, Wapendeni adui zenu, waombeeni wanaowaudhi, ili mpate kuwa wana wa Baba yenu aliye mbinguni; maana yeye huwaangazia jua lake waovu na wema, huwanyeshea mvua wenye haki na wasio haki.”

 

Luka 23:33-34 “Na walipofika mahali paitwapo Fuvu la Kichwa, ndipo walipomsulibisha yeye, na wale wahalifu, mmoja upande wa kuume, na mmoja upande wa kushoto. Yesu akasema, Baba, uwasamehe, kwa kuwa hawajui watendalo. Wakagawa mavazi yake, wakipiga kura.”

 

3.       Endelea kutenda mema -  Lengo kubwa la shetani wakati mwingine kukushambulia kupitia watu ni ili wewe uwe mtu mbaya, uone kuwa kila unapotenda mema unalipwa mabaya kwa hiyo unaamua kufunga milango yako ya wema na kuwa mbinafsi lakini neno la Mungu linatutaka tuendelee kuwa washindi kwa kutenda mema, kadiri unavyoendelea kuwa mwema na kutenda haki wema wako utawanyamazisha maadui zako na kila ubaya wanaokuzushia

 

Warumi 12:19 “Wapenzi, msijilipize kisasi, bali ipisheni ghadhabu ya Mungu; maana imeandikwa, Kisasi ni juu yangu mimi; mimi nitalipa, anena Bwana.Lakini, Adui yako akiwa na njaa, mlishe; akiwa na kiu, mnyweshe; maana ufanyapo hivyo, utampalia makaa ya moto kichwani pake. Usishindwe na ubaya, bali uushinde ubaya kwa wema.”

 

4.       Endelea kupiga kazi, endelea kumtumikia Mungu – Wakati maadui zako wanapokushambulia wewe ongezea viwango vya kumtumikia Mungu na kufanya kazi kwa bidii, kadiri unavyoendelea kumtumikia Mungu kwa bidii Mungu ataendelea kukubariki na kazi unazozifanya zitatangaza kile kitu Mungu ameweka ndani yako,  na kuudhihirishia ulimwengu kuwa yeye yuko na wewe, unapoendelea kumtumikia Mungu kwa nguvu Baraka zako zinaendelea kuongezeka na adui zako wanaendelea kuwekwa uchi neno la Mungu linasema adui zako watakuonyesha maungo yao, yaani uchi zao zitafunuliwa, aibu zao zitawekwa wazi, utupu wao utahukumiwa na kazi unazozifanya wataaibika na kazi yako itasema si biblia imesema kwa matunda yao mtawatambua, je mti mbaya unaweza kuzaa matunda mema?

 

Kutoka 23:25-27 “Nanyi mtamtumikia BWANA, Mungu wenu, naye atakibarikia chakula chako, na maji yako; nami nitakuondolea ugonjwa kati yako. Hapatakuwa na mwenye kuharibu mimba, wala aliye tasa, katika nchi yako; na hesabu ya siku zako nitaitimiza.Nitatuma utisho wangu utangulie mbele yako, nami nitawafadhaisha watu wote utakaowafikilia, nami nitawafanya hao adui zako wote wakuonyeshe maungo yao.”   

 

Yohana 10:37-38 “Kama sizitendi kazi za Baba yangu, msiniamini; lakini nikizitenda, ijapokuwa hamniamini mimi, ziaminini zile kazi; mpate kujua na kufahamu ya kuwa Baba yu ndani yangu, nami ni ndani ya Baba.”

 

Chuki kutoka kwa wapendwa na watumishi wenzako haimaanishi kuwa Mungu amekuacha bali inakufundisha kuelewa maswala ya kiroho, sio kuwa wakati wote watu watakuchukia kwa sababu wewe ni muovu hapana bali kwa sababu wao ni dhaifu kiroho, Mungu anakufundisha uwezo wa kuvumilia kabla ya kukuinua kukubariki na kukutumia, Mungu anakufundisha kuwa kama Yeye, wewe hujasahaulika, wewe hujashindwa wewe uko sawa na Daudi, uko sawa na Yusufu unafafanana na Yesu  na  ndio maana unachukiwa bila ya sababu za halali, wewe utakuwa kiroho vizuri zaidi, ukiyamudu hayo machungu yote ujue wazi kuwa thawabu yako ni kubwa sana mbinguni


Mathayo 5:11-12 “Heri ninyi watakapowashutumu na kuwaudhi na kuwanenea kila neno baya kwa uongo, kwa ajili yangu. Furahini, na kushangilia; kwa kuwa thawabu yenu ni kubwa mbinguni; kwa maana ndivyo walivyowaudhi manabii waliokuwa kabla yenu.”              

 

Na. Rev. Innocent Samuel Kamote


Mkuu wa wajenzi mwenye Hekima.