Jumapili, 15 Februari 2026

Sauti ya kijana huko jangwani!


Mwanzo 21:14-20 “Ibrahimu akaamka asubuhi na mapema akatwaa mkate na kiriba cha maji, akampa Hajiri akimtwika begani pake, na kijana, akamruhusu; naye akatoka, akapotea katika jangwa la Beer-sheba. Yale maji yakaisha katika kiriba, akamlaza kijana chini ya kijiti kimoja. Akaenda akakaa akimkabili, mbali naye kadiri ya mtupo wa mshale; maana alisema, Nisimwone kijana akifa; naye akakaa akimkabili, akapaza sauti yake, akalia. Mungu akasikia sauti ya kijana. Malaika wa Mungu akamwita Hajiri kutoka mbinguni, akamwambia, Una nini, Hajiri? Usiogope, maana Mungu amesikia sauti ya kijana huko aliko. Ondoka, ukamwinue kijana, ukamshike mkononi mwako, kwa kuwa nitamfanya kuwa taifa kubwa. Mungu akamfumbua macho, naye akaona kisima cha maji; akaenda akakijaza kiriba maji, akamnywesha kijana. Mungu akawa pamoja na huyo kijana, naye akakua, akakaa katika jangwa, akawa mpiga upinde.”




Utangulizi:

Kama kuna mojawapo ya matukio magumu sana duniani ni pamoja na tukio la kukataliwa na baba yako aliyekuzaa, maumivu ya kukataliwa na baba yanaweza kusababisha jeraha lisiloweza kukoma, hofu, kukosa kujiamini na kutelekezwa, jambo ambalo linaweza kupunguza kwa kiwango kikubwa uwezo wa kuwaamini watu, lakini pia linaweza kusababisha msongo wa mawazo, kushindwa kujitambua na kutokujitosheleza, inahitajika nguvu ya ziada sana kuweza kuwa kawaida na kuishinda hali ya kukataliwa, Lazima uwe na kitu cha ziada kuweza kujijenga kuwa unastahili na kujikomboa kutoka katika maumivu hayo ya kihisia kwani hali hii inazalisha hali ya kutaka  kujithibitisha.

Haya ndiyo yaliyomkuta Ishmael baada ya kufukuzwa nyumbani kwa baba yake ambaye kimsingi alikuwa tajiri sana wa mifugo fedha na dhahabu, lakini inaelezwa kuwa Ishamel na mama yake walitolewa mikono mitupu, wakipewa maji na mkate tu na hawakuwa hata na mtu wa kuwasindikiza, wala hawakuwa na chakula hata cha akiba, bali tupu.

Mwanzo 13:21-3 “Abramu akapanda kutoka Misri, yeye, na mkewe, na kila alichokuwa nacho, na Lutu pamoja naye, mpaka kusini. Naye Abramu alikuwa ni tajiri sana kwa mifugo, kwa fedha, na kwa dhahabu. Akaendelea kusafiri kutoka kusini mpaka Betheli, mahali pale palipokuwapo hema yake kwanza kati ya Betheli na Ai;”

Abrahamu alikuwa ni mtu aliyefanikiwa sana, alikuwa na makundi makubwa ya mifugo, wasimamizi, wafanyakazi, utajiri mkubwa wa fedha na dhahabu, lakini alikuwa ni mtu mwenye jeshi kali lililoweza kupigana vita na wafalme wakubwa katika vita, na moja ya vita maarufu aliyopigana na kuteka nyara ni vita iitwayo “opereshini Lutu”, ambapo alikwenda kupigana kumuokoa Lutu, Jeshi hilo lilikuwa na makomandoo 318 ambao walikuwa wamefunzwa vizuri  

Mwanzo 14:5-16 “Na mwaka wa kumi na nne akaja Kedorlaoma na wafalme waliokuwa pamoja naye, wakawapiga Warefai katika Ashteroth-karnaimu, na Wazuzi katika Hamu, na Waemi katika Shawe-kiryathaimu,na Wahori katika mlima wao Seiri, mpaka Elparani iliyo karibu na jangwa. Kisha wakarudi wakaja mpaka Enmisfati, ndio Kadeshi, wakapiga nchi yote ya Waamaleki, na Waamori waliokaa Hasason-tamari. Mfalme wa Sodoma, na mfalme wa Gomora, na mfalme wa Adma, na mfalme wa Seboimu, na mfalme wa Bela, ndio Soari, wakatoka wakapanga vita panapo bonde la Sidimu; wapigane na Kedorlaoma mfalme wa Elamu, na Tidali mfalme wa Goimu, na Amrafeli mfalme wa Shinari, na Arioko mfalme wa Elasari, wafalme wanne juu ya wale watano. Na bonde la Sidimu lilikuwa limejaa mashimo ya lami. Nao wafalme wa Sodoma na Gomora wakakimbia, wakaanguka huko, nao waliosalia wakakimbia milimani. Wakachukua mali zote za Sodoma na Gomora na vyakula vyao vyote, wakaenda zao. Wakamtwaa Lutu, mwana wa nduguye Abramu, aliyekaa huko Sodoma, na mali yake, wakaenda zao. Mtu mmoja aliyeponyoka akaenda, akampasha habari Abramu Mwebrania; naye amekaa panapo mialoni ya Mamre, yule Mwamori, ndugu ya Eshkoli, na ndugu ya Aneri, na hao walikuwa wamepatana na Abramu. Abramu aliposikia ya kwamba nduguye ametekwa mateka, akawapa silaha vijana wake, waliozaliwa katika nyumba yake, watu mia tatu na kumi na wanane, akawafuata mpaka Dani. Akajipanga apigane nao usiku, yeye na watumwa wake, akawapiga, akawafukuza mpaka Hoba, ulioko upande wa kushoto wa Dameski. Naye akarudisha mali zote, akamrudisha na Lutu nduguye na mali zake, na wanawake pia, na watu.”

Kwa hiyo unapata picha jinsi Abrahamu alivyokuwa mtu mkubwa sana mwenye uwezo mwingi na utajiri na mtu mwenye kumiliki Jeshi lake binafsi, na alipigana na wafalme zaidi ya watano na kuwashinda na kumrejesha Lutu na familia yake nyumbani na mifugo na mali zake sasa anamfukuza mtoto wa kumzaa mwenyewe tena mikono mitupu! Kwa mujibu wa  vitabu vya mafafanuzi ya kiyahudi na tamaduni zake viitwavyo “Talmudi” na “Midrashi” vinaeleza hivi kwa lugha ya kiingereza kuhusu Ishamel “Ishmael’s experience upon being sent away by Abraham was one of severe trauma, desperation and existential abandonment” kwa tafasiri yangu isiyo rasmi wanasema swala la kufukuzwa kwa Ishmael na Abrahimu lilikuwa ni mojawapo ya tukio baya, la kusikitisha, na kutelekezwa kikatili, kusikokuwa kwa kawaida” mtu tajiri mwenye uwezo mkubwa usiokuwa wa kawaida anamtoa mtoto wake wa kumzaa mikono mitupu bila kujali hali yake ya baadaye itakuwaje hata kama alizaliwa na mjakazi!

Mgogoro ulianza wakati Sara alipomshuhudia Ishmael akimdhihaki Isaka siku ile alipofanyiwa ibada ya shukurani kwaajili ya muujiza ule mkubwa wa kuzaliwa kwake Isaka na kuachishwa kunyonya

Mwanzo 21:6-10 “Sara akasema, Mungu amenifanyia kicheko; kila asikiaye atacheka pamoja nami. Akasema, N'nani angemwambia Ibrahimu, Sara atanyonyesha wana? Maana nimemzalia mwana katika uzee wake. Mtoto akakua, akaachishwa kunyonya; Ibrahimu akafanya karamu kuu siku ile Isaka alipoachishwa kunyonya. Sara akamwona yule mwana wa Hajiri Mmisri, ambaye alimzalia Ibrahimu, anafanya dhihaka. Kwa hiyo akamwambia Ibrahimu, Mfukuze mjakazi huyu na mwanawe, maana mwana wa mjakazi hatarithi pamoja na mwanangu, Isaka.”

Jambo hili halikumfurahisha Abraham, hata hivyo Mungu alimwambia Abrahamu afanye kile ambacho Sara ameagiza

Mwanzo 21:11.-12 “Na neno hilo lilikuwa baya sana machoni pa Ibrahimu, kwa ajili ya mwanawe. Mungu akamwambia Ibrahimu, Neno hili lisiwe baya machoni pako, kwa ajili ya huyo mwana, na huyo mjakazi wako. Kila akuambialo Sara, sikiza sauti yake, kwa maana katika Isaka uzao wako utaitwa.”

Jambo hili linamuweka Ishmael na mama yake katika wakati mbaya sana sasa wanapitia hali ngumu na ya uchungu sana, tutaliangalia somo hizi Sauti ya kijana Jangwani kwa kuzingatia vipengele vitatu vifuatavyo:-

·         Maumivu ya kukataliwa

·         Sauti ya kijana huko jangwani

·         Mungu anamkumbuka kijana huko jangwani

Maumivu ya kukataliwa

Tunawaona Ishmael na mama yake wakiwa jangwani maji yanawaishia na mkate unamalizika hali ya mauti sasa ndiyo inayomzunguka mtoto, akiwa ni kijana wa miaka 16 tu ambaye alilelewa maisha ya kudekezwa kama mtoto pekee nyumbani ghafla maisha yanabadilika na anatupwa jangwani, moyoni ana maumivu makali ya kutupwa na kukataliwa anajiona kama mtu asiye na bahati na ambaye amesalitiwa na baba yake na sio hivyo tu ametelekezwa, Ishmael na mama yake wanachanganyikiwa wamefukuzwa nyumbani nani kama wanatakiwa kuja kufia jangwani.

Mwanzo 21:14-16 “Ibrahimu akaamka asubuhi na mapema akatwaa mkate na kiriba cha maji, akampa Hajiri akimtwika begani pake, na kijana, akamruhusu; naye akatoka, akapotea katika jangwa la Beer-sheba. Yale maji yakaisha katika kiriba, akamlaza kijana chini ya kijiti kimoja. Akaenda akakaa akimkabili, mbali naye kadiri ya mtupo wa mshale; maana alisema, Nisimwone kijana akifa; naye akakaa akimkabili, akapaza sauti yake, akalia.”  

Maji yamekwisha chakula pia kimeisha ni jambo la kushangaza kuwa wanatupwa hata bila ya chakula cha akiba na wanapotelea katika jangwa anakabiliwa na kiu anachoka na wamekuwa dhaifu, mama yake anamuweka katika kichaka cha nyikani anakimbia mbali ili asimuone mtoto wake anapokata roho ana wasiwasi na hofu ya kuona mauti ikimmaliza mwanae

Kijana anajutia kumdhihaki Isaka anatambua kosa lake ambalo sasa linamletea mateso, anakuwa imara na anapokea mabadiliko toba yake inaonekana kwa ushahidi kuwa alimalizana vizuri na baba yake kwani alielewa upumbavu wake na sasa alimuheshimu Isaka kwa mujibu wa masimulizi ya marabi wa kiyahudi “Rabbinic tradition” (Genesis Rabbah) adhabu hii ilileta toba na mabadiliko makubwa kwani alikuja kumzika baba yake kwa heshima akiwa na Isaka ona:-

Mwanzo 25:8-10. “Ibrahimu akafariki, naye akafa katika uzee mwema, mzee sana, ameshiba siku, akakusanyika kwa watu wake. Isaka na Ishmaeli wanawe wakamzika katika pango ya Makpela, katika shamba la Efroni bin Sohari Mhiti, lielekealo Mamre. Katika lile shamba alilolinunua Ibrahimu kwa wazawa Hethi, huko ndiko alikozikwa Ibrahimu na Sara mkewe.”

Ndugu yangu kutelekezwa hakumaanishi kuwa umefika mwisho wa maisha, kutelekezwa hakumaanishi kuwa Mungu amemalizana na wewe watu wanaweza kukukataa na kukutelekeza lakini Mungu kamwe hawezi kufanya hivyo, Mikono yake bado iko wazi na anaweza kukupokea, Jangwa ndilo linalomfanya mtu kuwa imara na kuacha upumbavu wake, Jangwa lilikuwa eneo la somo kwa Ishmael, alijifunza kusamehe hakumuwekea kinyongo baba yake  Mungu aliisikiliza sauti yake kule jangwani  na alikuwa amemuandalia kisima kizuri cha maji ambayo yangeokoa uhai wake na kumfanya kuwa kijana shujaa,

Zaburi 34:6-9 “Maskini huyu aliita, Bwana akasikia, Akamwokoa na taabu zake zote.Malaika wa Bwana hufanya kituo, Akiwazungukia wamchao na kuwaokoa. Onjeni mwone ya kuwa Bwana yu mwema; Heri mtu yule anayemtumaini. Mcheni Bwana, enyi watakatifu wake, Yaani, wamchao hawahitaji kitu.”

Sauti ya kijana huko jangwani

Mwanzo 21:17-21 “Mungu akasikia sauti ya kijana. Malaika wa Mungu akamwita Hajiri kutoka mbinguni, akamwambia, Una nini, Hajiri? Usiogope, maana Mungu amesikia sauti ya kijana huko aliko. Ondoka, ukamwinue kijana, ukamshike mkononi mwako, kwa kuwa nitamfanya kuwa taifa kubwa. Mungu akamfumbua macho, naye akaona kisima cha maji; akaenda akakijaza kiriba maji, akamnywesha kijana. Mungu akawa pamoja na huyo kijana, naye akakua, akakaa katika jangwa, akawa mpiga upinde. Akakaa katika jangwa la Parani; mama yake akamtwalia mke katika nchi ya Misri.”

Jina Ishmael maana yake Mungu amesikia kilio changu, Mungu alisikia kilio cha mtoto, Mungu sio dhalimu hata pale inapoonekana kuwa ndoto zako zimezikwa na unabii kukuhusu umefukiwa katika mchanga, Mungu ataendelea kuwa mwaminifu kwa watu wake na neno lake mbingu ziliitikia sauti jangwani, kijana kweli alikuwa amefukuzwa nyumbani lakini hakuwa amefukuzwa kutoka kwenye uwepo wa Mungu, Mungu alimwambia Hajiri usiogope, na Mungu aliyafunua macho yake na akaona kisima chenye maji, kisima ambacho kimsingi kilikuwapo pale  tayari, watu wengi sio kuwa Mungu amewaacha bali watu wengi wamefungwa macho wasione fursa na ndio maana wanalia, Ni kazi ya Roho wa Mungu kukufunulia fursa, hauna sababu ya kulia lakini unapaswa kuinua macho yako uone.

Unaweza kukataliwa, kuteswa na kufukuzwa na hata kuwekwa nje ya mtandao “Systems” unaweza kutupwa na baba yako wa kiroho kabisa na unaweza usijaliwe na wale waliotakiwa kukujali lakini hili ndio tunalojifunza kuwa kama Mungu nanaweza kusikia kilio jangwani taabu yako haiwezi kunyamaziwa mbinguni, inaweza kunyamaziwa na wanadamu lakini Mungu hawezi kunyamaza, unaweza kufukuzwa, unaweza kuwa na kiu na unaweza hata kusahaulika , lakini Mungu hawezi kuacha kukusikia, utembeleo wa malaika hauzuiliki na hali, na uhakika wa maisha yako ya baadae uko mikononi mwa Mungu, maji yanaweza kuisha, mkate unaweza kumalizika, milango inaweza kufunga na watu wanaweza kukaa kimya lakini Mungu anayemsikiliza Ishmael yuko hata leo yeye hatakuacha ufie jangwani atakufunulia macho yako na atakuelekeza nini cha kufanya, Mungu alikuwa pamoja na Ishamel Mungu hana upendeleo haijalishi wewe ni wa mwanamke muungwana au wa mjakazi.

Mungu anamkumbuka kijana huko jangwani

Mungu alikumbuka agano lake alilolifanya na mama yake kuhusu kijana aliahidi kuwa angemfanya taifa kubwa na kwa sababu hiyo kufa jangwani haukuwa mpango wa Mungu, Mungu alikumbuka mpango wake na Mungu alisikia kilio cha Ishmael Mungu akamkumbuka kijana huko jangwani!

Mwanzo 16:6-11 “Naye Abramu akamwambia Sarai, Tazama, mjakazi wako yu mkononi mwako, mtendee lililo jema machoni pako. Sarai akamtesa, naye akakimbia kutoka mbele yake. Malaika wa BWANA akamwona kwenye chemchemi ya maji katika jangwa, chemchemi iliyoko katika njia ya kuendea Shuri. Akamwambia, Hajiri, wewe mjakazi wa Sarai, unatoka wapi, nawe unakwenda wapi? Akanena, Nakimbia mimi kutoka mbele ya bibi yangu Sarai. Malaika wa BWANA akamwambia, Rudi kwa bibi yako, ukanyenyekee chini ya mikono yake. Malaika wa BWANA akamwambia, Hakika nitauzidisha uzao wako, wala hautahesabika kwa jinsi utakavyokuwa mwingi. Malaika wa BWANA akamwambia, Tazama! Wewe una mimba, utazaa mwana wa kiume, nawe utamwita jina lake Ishmaeli, maana BWANA amesikia kilio cha mateso yako.”

Mungu alizungumza na Hajiri wakati wa changamoto, Mungu huleta ufumbuzi wakati wa changamoto, Mungu alimwambia asiogope, na Mungu alimfunulia macho kuona kisima cha maji, Mungu alikuwa ameahidi kumfanya Ishamel kuwa taifa kubwa na Ishamel akawa mkuu mno na wafalme 12 walitokea katika viuno vyake

Mwanzo 25:12-17 “Hivi ndivyo vizazi vya Ishmaeli, mwana wa Ibrahimu, ambaye Hajiri, Mmisri, mjakazi wa Sara, alimzalia Ibrahimu. Na haya ndiyo majina ya wana wa Ishmaeli, kwa majina yao, na kwa vizazi vyao. Mzaliwa wa kwanza wa Ishmaeli, ni Nebayothi, na Kedari, na Abdeeli, na Mibsamu, na Mishma, na Duma, na Masa, na Hadadi, na Tema, na Yeturi, na Nafishi, na Kedema. Hao ndio wana wa Ishmaeli, na hayo ni majina yao, katika miji yao, na katika vituo vyao, maseyidi kumi na wawili kwa kufuata jamaa zao. Na hii ndiyo miaka ya maisha ya Ishmaeli, miaka mia na thelathini na saba. Akakata roho, akafa, akakusanyika kwa watu wake.”

Mungu ndiye anayeshikilia maisha yako, mipango yako iko katika mikono yake tangu kuwekwa kwa misingi ya ulimwengu, hakuna bahati mbaya yeye ni muumba mwenye upendo, kila mtu duniani yuko katika mpango wake na ni yeye ndiye anayeziongoza njia zako, na makusudi yake kwako atayatimiza mwenyewe katika mpango wake haijalishi ni vikwazo gani utakutana navyo au ni giza gani liko mbele yako hiyo haimaanishi kuwa Mungu amekuacha ni swala la kufumba na kufumbua tu amini mchakato wa Mungu “trust the process” yeye atakulinda, atakuongoza atakuweka katika njia iliyo sahihi, hakuna anayeweza kuuzuia mpango wake wala makusudi yake, Mungu anaweza kuwainua watu kwaajili yako na wakakutendea mema watakusaidia kulifikia kusudi lako haijalishi watu wamekuchezea kiasi gani lakini Mungu ni mwenye nguvu kuliko wao, Je uko kwenye jangwa gani? Mungu anaisikia sauti yako, hutafia jangwani yeye bado hajamalizana na wewe, Mungu ana ahadi na wewe na ni lazima aitimize!

 

Na Rev. Innocent Samuel Kamote

 

Mkuu wa wajenzi mwenye Hekima 

Jumapili, 8 Februari 2026

Kanuni za kuwekea/kuwekewa Mikono:


Matendo 13:1-3Na huko Antiokia katika kanisa lililokuwako palikuwa na manabii na waalimu, nao ni Barnaba, na Simeoni aitwaye Nigeri, na Lukio Mkirene, na Manaeni aliyekuwa ndugu wa kunyonya wa mfalme Herode, na Sauli. Basi hawa walipokuwa wakimfanyia Bwana ibada na kufunga, Roho Mtakatifu akasema, Nitengeeni Barnaba na Sauli kwa kazi ile niliyowaitia. Ndipo wakiisha kufunga na kuomba, wakaweka mikono yao juu yao, wakawaacha waende zao.”




Utangulizi.

Leo nataka kuzungumzia mojawapo ya ibada ya muhimu na ya msingi na ya zamani sana, katika utamaduni wa kanisa na kimaandiko na hii ni ibada ya kuwekea mikono au kuwekewa mikono, Ibada hii ni ya muhimu kwa sababu ni ya kimaandiko na inaendelea kutenda kazi hata katika siku zetu, ingawa kuna umuhimu wa kujikumbusha ili tuweze kuwa na uelewa wa kina na mapana na marefu kuhusu kuwekea au kuwekewa mikono, kuwekea au kuwekewa mikono kuna uwezo wa kuruhusu neema ya Mungu juu ya maisha ya huduma na utumishi wa mtu, aidha pia mikono inahusika katika kupitisha Baraka, neema na uponyaji wa mwili nafsi na roho kwa hiyo uko umuhimu wa Kanisa kuwa na uelewa.

Kumbukumbu 34:9 “Na Yoshua, mwana wa Nuni, alikuwa amejaa roho ya hekima; maana Musa alikuwa amemwekea mikono yake juu yake; wana wa Israeli wakamsikiliza, wakafanya kama Bwana alivyomwamuru Musa.”

2Timotheo 1:6-7 “Kwa sababu hiyo nakukumbusha, uichochee karama ya Mungu, iliyo ndani yako kwa kuwekewa mikono yangu. Maana Mungu hakutupa roho ya woga, bali ya nguvu na ya upendo na ya moyo wa kiasi.”

Kwa msingi huu leo tutachukua muda kujifunza kwa kina na mapana na marefu kuhusu swala zima la kuwekea au kuwekewa mikono, ambalo kimsingi ni lazima liambatane na maombi kama ilivyo kwenye swala la kufunga, au kupaka mafuta vilevile kuweka mikono huendana na kuomba au kusema maneno yanayoambatana na kusudi la kuwekea mikono huko, ili kulitungua kusudi hilo kutoka katika ulimwengu wa roho na mkao wa Moyo kwa kusudi la kutimiza mapenzi ya Mungu, tutajifunza somo hili Kanuni za kuwekea au kuweka Mikono kwa kuzingatia vipengele vifuatavyo:-


·         Asili ya kuwekea au kuwekewa mikono.

·         Makusudi ya ibada ya kuwekea au kuwekewa mikono

·         Kanuni za kuwekea au kuwekewa mikono


Asili ya kuwekea au kuwekewa mikono.

Kuwekea mikono au kuwekewa mikono “laying on of hands” ni tendo la ibada la kimwili ambapo mtu au watu au kikundi cha watu huweka mikono inayoambatana na maombi juu ya wengine kama ishara ya kiroho yenye lengo la kubariki, kuhamisha mamlaka, kuweka wakfu viongozi, kuwatenga watu kwaajili ya huduma, kufanya maombezi ya uponyaji, kuchochea karama, kurithisha Baraka na kutambulisha na ubatizo wa Roho Mtakatifu, Tendo hili ingawa linafanyika katika mwili kiibada linaunganisha mamlaka ya Mungu ndani ya Mwanadamu anayepokea kusudi hilo. Ni ishara inayoonekana ya neema ya Mungu isiyoonekana na uweza wa Roho Mtakatifu.

Tendo la kuwekea mikono kwa asili linaonekana katika maandiko ya Kiebrania likitajwa kwa kiebrania kwa neno “Semikhah” kwa kiingereza “succession” kwa kiwahili ni kurithisha kwa mfululizo, mfano kutoka katika uongozi wa mtu mmoja kwenda katika uongozi wa mtu mwingine kwa kurithishana kwa Amani au kwa lengo la kuendeleza au kusaidia au kupitisha mfano Musa alipozidiwa na majukumu ya kichungaji katika kanisa lililokuwako Jangwani alichagua wazee sabini “70” kwa maelekezo ya Mungu na kuwawekea mikono na kwa tendo hilo sehemu ya utendaji wa Musa  iliwapata wazee wale sabini ili waweze kumsaidia majukumu yake.

Hesabu 11:24-29 “Musa akatoka, akawaambia watu maneno ya Bwana; akawakutanisha watu sabini miongoni mwa wazee wa watu, akawaweka kuizunguka Hema. Ndipo Bwana akashuka ndani ya wingu, akanena naye, akatwaa sehemu ya roho iliyokuwa juu ya Musa, akaitia juu ya wale wazee sabini; ikawa, roho hiyo ilipowashukia, wakatabiri, lakini hawakufanya hivyo tena. Lakini watu wawili walisalia kambini, jina la mmoja aliitwa Eldadi, na jina la wa pili aliitwa Medadi; na roho ile ikawashukia; nao walikuwa miongoni mwao walioandikwa, lakini walikuwa hawakutoka kwenda hemani; nao wakatabiri kambini. Mtu mmoja kijana akapiga mbio, akaenda akamwambia Musa, akasema, Eldadi na Medadi wanatoa unabii kambini. Yoshua mwana wa Nuni, mtumishi wa Musa tangu ujana wake, akajibu akasema, Ee bwana wangu Musa, uwakataze. Musa akamwambia, Je! Umekuwa na wivu kwa ajili yangu; ingekuwa heri kama watu wote wa Bwana wangekuwa manabii na kama Bwana angewatia roho yake.”

Hesabu 27:16-20 “Bwana, Mungu wa roho za wenye mwili wote, na aweke mtu juu ya mkutano, atakayetoka mbele yao, na kuingia mbele yao; atakayewaongoza watokapo, na kuwaleta ndani; ili mkutano wa Bwana wasiwe kama kondoo wasio na mchungaji. Bwana akamwambia Musa, Mtwae Yoshua, mwana wa Nuni, mtu mwenye roho ndani yake, ukamwekee mkono wako; kisha ukamweke mbele ya Eleazari kuhani, na mbele ya mkutano wote; ukampe mausia mbele ya macho yao. Nawe utaweka juu yake sehemu ya heshima yako, ili mkutano wote wa wana wa Israeli wapate kutii.”

Asili nyingine ya kuwekea mikono ilifanywa na makuhani kwa kuweka mikono yao juu ya mnyama kwaajili ya sadaka ya kuteteketezwa ya dhambi, Kuhani angeweka mikono yake juu ya mnyama kama ishara ya kusafirisha dhambi ya hatia kutoka kwa mwanadamu anayeombewa au kufanyiwa upatanishi kuelekea kwa mnyama huyo kisha angechinjwa na kuteketezwa kama ishara ya msamaha wa dhambi kutoka kwa muathirika, aidha tukio kama hili lilifanywa na kuhani mkuu kwaajili ya dhambi za taifa kwa mwanambuzi wa hazazeli mbuzi wa kafara ambaye angechukua uovu wa watu na kupotelea nao jangwani.

Walawi 1:2-5 “Nena na wana wa Israeli, uwaambie, Mtu wa kwenu atakapomtolea BWANA matoleo, mtatoa matoleo yenu katika wanyama wa mifugo, katika ng'ombe na katika kondoo. Matoleo yake kwamba ni sadaka ya kuteketezwa ya ng'ombe, atatoa ng'ombe mume mkamilifu; ataleta mlangoni pa hema ya kukutania, ili akubaliwe mbele ya BWANA. Kisha ataweka mkono wake juu ya kichwa cha hiyo sadaka ya kuteketezwa; nayo itakubaliwa kwa ajili yake, ili kufanya upatanisho kwa ajili yake. Naye atamchinja huyo ng'ombe mbele ya BWANA; kisha wana wa Haruni, hao makuhani, wataileta karibu hiyo damu, na kuinyunyiza damu yake kando-kando katika madhabahu iliyo hapo mlangoni pa hema ya kukutania.”

Walawi 16:21-22 “Na Haruni ataweka mikono yake miwili juu ya kichwa cha yule mbuzi aliye hai, na kuungama juu yake uovu wote wa wana wa Israeli, na makosa yao, naam, dhambi zao zote; naye ataziweka juu ya kichwa chake yule mbuzi, kisha atampeleka aende jangwani kwa mkono wa mtu aliye tayari.Na yule mbuzi atachukua juu yake uovu wao wote, mpaka nchi isiyo watu; naye atamwacha mbuzi jangwani.”

Asili nyingine ya tendo la kuwekea mikono ni kwaajili ya urithi au kuhamisha Baraka, ambapo tunaona Yakobo akiwarithi watoto wa Yusufu na kuwa wa kwake, huku akiweka mkono wa kuume juu ya mdogo na mkono wa kushoto juu ya mkubwa ili kumuinua Efraimu na kumshusha Manase katika mbaraka wake.

Mwanzo 48:13-16 “Yusufu akawaweka wote wawili, Efraimu katika mkono wake wa kuume, kuelekea mkono wa kushoto wa Israeli; na Manase katika mkono wake wa kushoto, kuelekea mkono wa kuume wa Israeli, akawasogeza karibu naye. Israeli akanyosha mkono wake wa kuume akauweka juu ya kichwa cha Efraimu, aliyekuwa mdogo, na mkono wake wa kushoto akauweka juu ya kichwa cha Manase, huku akijua atiavyo mikono; maana Manase ndiye aliyezaliwa kwanza. Akambariki Yusufu, akasema, Mungu ambaye baba zangu, Ibrahimu na Isaka, walienenda mbele zake, yeye Mungu aliyenilisha, maisha yangu yote, hata siku hii ya leo, naye Malaika aliyeniokoa na maovu yote, na awabariki vijana hawa; jina langu na litajwe juu yao, na jina la baba zangu, Ibrahimu na Isaka; na wawe wingi wa watu kati ya nchi.”

Ibada ya kuwekea mikono imekuwa na matumizi makubwa sana katika nyakati za agano jipya katika mazingira mbalimbali, Mwandishi wa kitabu cha Waebrania anayataja mafundisho ya msingi katika Kristo na mojawapo ya mafundisho haya ni pamoja na ibada za kuwekea mikono

Waebrania 6:1-3 “Kwa sababu hiyo, tukiacha kuyanena mafundisho ya kwanza ya Kristo, tukaze mwendo ili tuufikilie utimilifu; tusiweke msingi tena wa kuzitubia kazi zisizo na uhai, na wa kuwa na imani kwa Mungu, na wa mafundisho ya mabatizo, na kuwekea mikono, na kufufuliwa wafu, na hukumu ya milele. Na hayo tutafanya Mungu akitujalia.”

Makusudi ya ibada ya kuwekea au kuwekewa mikono.

Kwa ujumla unapolichunguza neno la Mungu kuhusu swala zima la kuwekea mikono utaweza kugundua kuwa ibada ya kuweka mikono au kuwekea mikono inafanyika kwa makusudi ya aina mbalimbali kama ifuatavyo:-

1.       Kwa kusudi la kubariki – Kimsingi moja ya sababu ya kuwekea mikono au kuwekewa mikono ni kwaajili ya Baraka za Mungu kwa yule anayewekewa mikono, Baraka za Mungu humfanya mtu awe na kibali na awe na mafanikio katika jambo analolifanya au analowekwa kulifanya kwaajili ya ufalme wa Mungu au kwa makusudi mengine, Mfano tunaona Yakobo akiweka mikono juu ya wajukuu zake ili kuwatakia Baraka za kinabii katika maisha yao, Lakini sio hivyo tu tunamuona bwana Yesu akiweka mikono juu ya watoto kwa kusudi la kuwabariki, aidha katika tamaduni za kikanisa pia watu wamekuwa wakiwawekea mikono wana ndoa wakati wa kuwatakia maisha mema katika ibada ya ndoa hili linaingia katika kundi hili la kuwekea mikono ili kuwabariki.

 

Mwanzo 48:20 “Akawabariki siku ile akasema, Katika ninyi Waisraeli watabariki, wakisema, Mungu na akufanye kama Efraimu na Manase. Akamweka Efraimu mbele ya Manase.”

 

Mathayo 19:13-15 “Ndipo akaletewa watoto wadogo ili aweke mikono yake juu yao na kuwaombea; wanafunzi wake wakawakemea. Lakini Yesu akasema, Waacheni watoto wadogo waje kwangu; wala msiwazuie; kwa maana walio mfano wa hao, ufalme wa mbinguni ni wao. Akaweka mikono yake juu yao, akatoka huko.”

 

Na kwa mujibu wa maelekezo ya kibiblia kama mtu atafanya ibada ya kubariki anayebariki anapaswa kuwa mkubwa kwa sababu Baraka hutoka kwa mkubwa kwenda kwa mdogo, kwa maana mtu huyo awe kuhani kwa maana ya mtumishi wa Mungu ambaye ni mkubwa kwa mamlaka aliyopewa na Mungu ya kubariki, lakini pia awe mkubwa kiumri, kwa hiyo ile mila ya kuwekewa mkono na mtoto mdogo kwa kuamini kuwa atakubariki ni kinyume na maelekezo ya kibiblia

 

Waebrania 7:1-7 “Kwa maana Melkizedeki huyo, mfalme wa Salemu, kuhani wa Mungu aliye juu, aliyekutana na Ibrahimu alipokuwa akirudi katika kuwapiga hao wafalme, akambariki; ambaye Ibrahimu alimgawia sehemu ya kumi ya vitu vyote; (tafsiri ya jina lake kwanza ni mfalme wa haki, tena, mfalme wa Salemu, maana yake, mfalme wa amani; hana baba, hana mama, hana wazazi, hana mwanzo wa siku zake, wala mwisho wa uhai wake, bali amefananishwa na Mwana wa Mungu); huyo adumu kuhani milele. Basi, angalieni jinsi mtu huyo alivyokuwa mkuu, ambaye Ibrahimu, baba yetu mkuu, alimpa sehemu ya kumi ya nyara. Na katika wana wa Lawi nao, wale waupatao ukuhani, wana amri kutwaa sehemu ya kumi kwa watu wao, yaani, ndugu zao, kwa agizo la sheria, ijapokuwa wametoka katika viuno vya Ibrahimu. Bali yeye, ambaye uzazi wake haukuhesabiwa kuwa umetoka kwa hao, alitwaa sehemu ya kumi kwa Ibrahimu, akambariki yeye aliye na ile ahadi. Wala haikanushiki kabisa kwamba mdogo hubarikiwa na mkubwa.”

 

2.       Kwa kusudi la kurithisha Uongozi – sababu nyingine ya ibada ya kuwekea mikono ni kwaajili ya kurithisha uongozi, “Semikhah” kwa kiingereza “succession hii hufanyika kwa kusudi la kumrithisha kiongozi kutoka kwa uongozi wa zamani kuja kwa uongozi mpya, wakati huu sehemu kama ile ya heshima au Roho yule yule aliyetenda kazi na kiongozi aliyepita hufanya kazi na kiongozi ajaye hata kama ni katika mtindo na mfumo wa aina nyingine na tabia nyingine lakini Roho ni yeye yule, Jambo hili linapofanyika sehemu ya heshima au mamlaka iliyokuweko juu ya kiongozi wa awali huamia kwa uongozi mpya na kumpa neema ya kutumika sawa na kiongozi wa awali au zaidi katika namna nyingine apendavyo Roho yeye yule.

 

Hesabu 27:16-20 “Bwana, Mungu wa roho za wenye mwili wote, na aweke mtu juu ya mkutano, atakayetoka mbele yao, na kuingia mbele yao; atakayewaongoza watokapo, na kuwaleta ndani; ili mkutano wa Bwana wasiwe kama kondoo wasio na mchungaji. Bwana akamwambia Musa, Mtwae Yoshua, mwana wa Nuni, mtu mwenye roho ndani yake, ukamwekee mkono wako; kisha ukamweke mbele ya Eleazari kuhani, na mbele ya mkutano wote; ukampe mausia mbele ya macho yao. Nawe utaweka juu yake sehemu ya heshima yako, ili mkutano wote wa wana wa Israeli wapate kutii.”

 

3.       Kwa kusudi la kuombea uponyaji na kufanya miujiza – Neno la Mungu linaonyesha kuwa ibada ya kuweka mikono pia inaweza kufanywa kwa nia ya kufanya maombezi na kuwaponya watu au kutumiwa na Mungu kwa njia ya miujiza, kwa hiyo utaweza kuona Yesu, na mitume kadhaa akiwemo Petro na Paulo na kadhalika ambao waliweza kuwaombea watu kwa kuwawekea mikono na wakapokea uponyaji, hata Yesu Kristo mwenyewe aliahidi ya kuwa wale wamuaminio watatumiwa kwa ishara mbalimbali ikiwa ni pamoja na kuweka mikono juu ya wagonjwa nao kupokea afya

 

Marko 6:4-5 “Yesu akawaambia, Nabii hakosi heshima, isipokuwa katika nchi yake mwenyewe, na kwa jamaa zake, na nyumbani mwake. Wala hakuweza kufanya mwujiza wo wote huko, isipokuwa aliweka mikono yake juu ya wagonjwa wachache, akawaponya.”

 

Matendo 9:11-12 “Bwana akamwambia, Simama, enenda zako katika njia iitwayo Nyofu, ukaulize katika nyumba ya Yuda mtu aitwaye Sauli, wa Tarso; maana, angalia, anaomba; naye amemwona mtu, jina lake Anania, akiingia, na kumwekea mikono juu yake, apate kuona tena.”

 

Matendo 28:7-8 “Karibu na mahali pale palikuwa na mashamba ya mkuu wa kisiwa, jina lake Publio; mtu huyu akatukaribisha kwa moyo wa urafiki, akatufanya wageni wake kwa muda wa siku tatu. Ikawa babaake Publio alikuwa hawezi homa na kuhara damu. Paulo akaingia kwake, akaomba, akaweka mikono yake juu yake, na kumpoza.”

 

Marko 16:17-18 “Na ishara hizi zitafuatana na hao waaminio; kwa jina langu watatoa pepo; watasema kwa lugha mpya; watashika nyoka; hata wakinywa kitu cha kufisha, hakitawadhuru kabisa; wataweka mikono yao juu ya wagonjwa, nao watapata afya.”

 

4.       Kwa kusudi la kumpokea Roho Mtakatifu – Uko ushahidi wa kimaandiko unaoshiria kuwa pamoja na kuweko kwa njia nyingi sana za watu kubatizwa kwa Roho Mtakatifu, inaonekana pia kuwa watu huweza kupokea Ubatizo wa Roho Mtakatifu kwa kuwekewa mikono  mfano

 

Matendo 8:14-19 “Na mitume waliokuwako Yerusalemu, waliposikia ya kwamba Samaria imelikubali neno la Mungu, wakawapelekea Petro na Yohana; ambao waliposhuka, wakawaombea wampokee Roho Mtakatifu; kwa maana bado hajawashukia hata mmoja wao, ila wamebatizwa tu kwa jina lake Bwana Yesu. Ndipo wakaweka mikono yao juu yao, nao wakampokea Roho Mtakatifu. Hata Simoni alipoona ya kuwa watu wanapewa Roho Mtakatifu kwa kuwekewa mikono ya mitume, akataka kuwapa fedha akisema, Nipeni na mimi uwezo huu, ili kila mtu nitakayemweka mikono yangu, apokee Roho Mtakatifu.”

 

Matendo 19:1-6 “Ikawa, Apolo alipokuwa Korintho, Paulo, akiisha kupita kati ya nchi za juu, akafika Efeso; akakutana na wanafunzi kadha wa kadha huko; akawauliza, Je! Mlipokea Roho Mtakatifu mlipoamini? Wakamjibu, La, hata kusikia kwamba kuna Roho Mtakatifu hatukusikia. Akawauliza, Basi mlibatizwa kwa ubatizo gani? Wakasema, Kwa ubatizo wa Yohana. Paulo akasema, Yohana alibatiza kwa ubatizo wa toba, akiwaambia watu wamwamini yeye atakayekuja nyuma yake, yaani, Yesu. Waliposikia haya wakabatizwa kwa jina la Bwana Yesu. Na Paulo, alipokwisha kuweka mikono yake juu yao, Roho Mtakatifu akaja juu yao; wakaanza kunena kwa lugha, na kutabiri.”

 

5.       Kwa kusudi la kuchochewa kwa karama – Wakati mwingine watu wa Mungu huwa na karama za Roho Mtakatifu ndani yao na vipawa mbalimbali lakini wakati mwingine karama zina tabia ya kujificha na hivyo mtu anaweza kuwekewa mikono na karama zikachochewa, tunapoendelea kumtumikia Mungu kama ilivyokuwa kwa Timotheo kwa muda Fulani wakati mwingine kuna uwezekano wa moto kupungua kutokana na changamoto mbalimbali Paulo alimtaka Timotheo ili kumuwekea mikono yake ili karama ziendelee kuwaka na kufanyakazi kwa kiwango cha juu Zaidi, karama pia huweza kuambukizwa ndani ya Mtu kwa kuwekewa mikono.

 

2Timotheo 1:6-7 “Kwa sababu hiyo nakukumbusha, uichochee karama ya Mungu, iliyo ndani yako kwa kuwekewa mikono yangu. Maana Mungu hakutupa roho ya woga, bali ya nguvu na ya upendo na ya moyo wa kiasi.”

 

1Timotheo 4:13-14 “Hata nitakapokuja, ufanye bidii katika kusoma na kuonya na kufundisha. Usiache kuitumia karama ile iliyomo ndani yako, uliyopewa kwa unabii na kwa kuwekewa mikono ya wazee.”

 

6.       Kwa kusudi la kusimika au kuweka wakfu viongozi wa kanisa na wale walioitwa katika wito maalumu – Viongozi wote makanisani wanapokuwa wameteuliwa au kuchaguliwa kwaajili ya kutimiza majukumu yao kadhaa waliyoitiwa na Roho Mtakatifu katika kanisa wanapaswa kuwekewa mikono ili wapokee neema ya kuwawezesha kubeba majukumu yao ya kikanisa au ya kitumishi kwa hiyo nyakati za kanisa la Kwanza kila walipoweka viongozi waliwawekea mikono.

 

Matendo 6:5-6 “Neno hili likapendeza machoni pa mkutano wote; wakamchagua Stefano, mtu aliyejaa imani na Roho Mtakatifu, na Filipo, na Prokoro, na Nikanori, na Timoni, na Parmena, na Nikolao mwongofu wa Antiokia; ambao wakawaweka mbele ya mitume, na walipokwisha kuomba wakaweka mikono yao juu yao.”

 

Matendo 13:1-3 “Na huko Antiokia katika kanisa lililokuwako palikuwa na manabii na waalimu, nao ni Barnaba, na Simeoni aitwaye Nigeri, na Lukio Mkirene, na Manaeni aliyekuwa ndugu wa kunyonya wa mfalme Herode, na Sauli. Basi hawa walipokuwa wakimfanyia Bwana ibada na kufunga, Roho Mtakatifu akasema, Nitengeeni Barnaba na Sauli kwa kazi ile niliyowaitia.Ndipo wakiisha kufunga na kuomba, wakaweka mikono yao juu yao, wakawaacha waende zao.”

 

7.       Huwezi kupokea roho chafu kwa kuwekewa mikono – Kumekuwepo na hofu kubwa sana kutoka kwa washirika na hata  baadhi ya watumishi wa Mungu mbali mbali wakionya kuwa uko uwezekano wa kupokea roho chafu kutokana na kuwekewa mikono, ni muhimu kufahamu kuwa Mkrito aliyeokoka vizuri na aliye muaminifu hawezi kamwe kupokea roho chafu kwa kuwekewa mikono  na mhudumu asiye mwaminifu, Mkristo aliyeokoka vema na kujazwa Roho Mtakatifu yeye ni Hekalu la Roho Mtakatifu na Roho wa Mungu anakaa ndani yake  

 

1Wakorintho 6:19 “Au hamjui ya kuwa mwili wenu ni hekalu la Roho Mtakatifu aliye ndani yenu, mliyepewa na Mungu? Wala ninyi si mali yenu wenyewe;”

 

Roho wa Mungu aliye ndani ya waamini au watu waliookoka ni mkuu kuliko yeye aliyeko katika ulimwengu huu kwa hiyo utabarikiwa na kufanikiwa kwa sababu ya tendo la kiungu na ibada inayofanyika ndani yako na sio kwa sababu ya hali ya mtumishi anayekuwekea mikono

 

1Yohana 4:4 “Ninyi, watoto wadogo, mwatokana na Mungu nanyi mmewashinda, kwa sababu yeye aliye ndani yenu ni mkuu kuliko yeye aliye katika dunia.”  

 

Yesu anaonyesha katika maandiko na mafundisho yake kuwa Mwamini hupewa kile anachokiomba na Mungu sio dhalimu kwamba akupe nyoka wakati umeomba samaki, au nge wakati umeomba yai na jiwe wakati umeomba Mkate Mungu huangalia moyo na atakupa sawasawa na uhitaji wa moyo wako na sio kwa sababu ya hali ya muhubiri au kiongozi anayekuwekea mikono

 

Luka 11:9-13 “Nami nawaambia, Ombeni, nanyi mtapewa; tafuteni, nanyi mtaona; bisheni, nanyi mtafunguliwa. Kwa kuwa kila aombaye hupokea; naye atafutaye huona; naye abishaye atafunguliwa. Maana ni yupi kwenu aliye baba, ambaye mwanawe akimwomba mkate, atampa jiwe au samaki, badala ya samaki atampa nyoka? Au akimwomba yai, atampa nge? Basi, ikiwa ninyi mlio waovu mnajua kuwapa watoto wenu vipawa vyema, je! Baba aliye mbinguni hatazidi sana kuwapa Roho Mtakatifu hao wamwombao?

 

Hana alipata mtoto katika wakati ambao watoto wa Eli yule kuhani walikuwa wameharibika na neno la Bwana lilikuwa adimu lakini kupitia maneno ya Eli na uhitaji wa mwanamke yule moyoni Mungu alijibu maombi nyake sawasawa na uhitaji wake kiyume kabisa na hali ya kuhani nyumbani mwa Bwana kwa hiyo hali ya kuhani sio changamoto ya kumfanya mtu asipokee kitu halisi anachikitamani na kukihitaji kutoka kwa Mungu.                        

 

Kanuni za kuwekea au kuwekewa mikono

Kama utakuwa umefuatilia vema somo hili utagundua kuwa kuweka mikono ni swala la kiroho na la Muhimu na kwa sababu hiyo lina kanuni zake, haliwezi kufanyika hovyo hovyo ama bila kufuata utaratibu na maelekezo ya kibiblia, kuwekea watu mikono ni njia ya kuruhusu neema ya Mungu kutoka kwa Roho Mtakatifu kupitia mikono yetu na kutimiza kusudi lake kwa mtu anayewekewa Mikono kwa hiyo tukio hili kama ilivyo kwa tukio la kupaka mafuta ni lazima lifanyike pamoja na maombi. Lakini pia kwa kuzingatia kanuni, kila anayeweka mikono ni lazima awe anajua anachokifanya na kujiuliza kwa nini anafanya na kusudi la kufanya hivyo, hivyo jambo hili lisifanyike ilimradi tu kwani ni ibada kamili.

Anayeweka mikono ni lazima awe anajua anachokifanya – Mtu anayeweka mikono anatakiwa awe anajua ni kwa nini anafanya hivyo, hili ni swala la kiroho na ni swala la maisha ni swala la kuinua mtu na kushusha mtu kwa hiyo anayeweka mikono anatakiwa kuwa na ujuzi na kile anachikifanya kwanza akiwa na ufahamu wa kawaida lakini pia kama ameongozwa na Mungu au roho ya kinabii kufanya hivyo ni lazima aelewe kusudi  linalomuongoza katika kuwekea mikono, Kwa mfano wakati Yakobo anamuwekea mkono wa kuume Efraimu na mkono wa kushoto Manase wakati Manase ndiye mkubwa na Efraimu ndiye mdogo, Yusufu alikuwa akielewa na kufikiri kuwa babaye anakosea lakini Yakobo alisisitiza kuwa anajua anachokifanya ona kumbe muwekewa mikono anapaswa kujua anachokifanya

Mwanzo 48:13-19 “Yusufu akawaweka wote wawili, Efraimu katika mkono wake wa kuume, kuelekea mkono wa kushoto wa Israeli; na Manase katika mkono wake wa kushoto, kuelekea mkono wa kuume wa Israeli, akawasogeza karibu naye. Israeli akanyosha mkono wake wa kuume akauweka juu ya kichwa cha Efraimu, aliyekuwa mdogo, na mkono wake wa kushoto akauweka juu ya kichwa cha Manase, HUKU AKIJUA ATIAVYO MIKONO; maana Manase ndiye aliyezaliwa kwanza. Akambariki Yusufu, akasema, Mungu ambaye baba zangu, Ibrahimu na Isaka, walienenda mbele zake, yeye Mungu aliyenilisha, maisha yangu yote, hata siku hii ya leo, naye Malaika aliyeniokoa na maovu yote, na awabariki vijana hawa; jina langu na litajwe juu yao, na jina la baba zangu, Ibrahimu na Isaka; na wawe wingi wa watu kati ya nchi. Yusufu alipoona kwamba babaye anaweka mkono wake wa kuume juu ya kichwa cha Efraimu, ikawa vibaya machoni pake. Akauinua mkono wa babaye auondoe katika kichwa cha Efraimu, ili auweke juu ya kichwa cha Manase. Yusufu akamwambia babaye, Sivyo, babangu, maana huyu ni mzaliwa wa kwanza; weka mkono wako wa kuume kichwani pake. Babaye akakataa, akasema, NAJUA, MWANANGU NAJUA, yeye naye atakuwa taifa, yeye naye atakuwa mkuu; lakini ndugu yake mdogo atakuwa mkubwa kuliko yeye, na uzao wake watakuwa wingi wa mataifa.”

Unaona utagundua katika kifungu hiki kuwa Yusufu na Yakobo walikuwa wanajua kuwa anayewekewa mikono wakati wa Baraka ikiwa atawezewa mkono wa kuume huyu ndiye atakuwa mkubwa na anayewekewa mkono wa kushoto atakuwa mdogo, hii ni kanuni ya kibiblia ambayo watumishi wengi wa Mungu huikosea hasa wakati wa kubariki maharusi kwa mfano unakuta wanaweka mikono hovyo na wakati mwingine mke anawekewa mkono wa kuume na mume anawekewa mkono wa kushoto hili ni kosa kubwa la kiufundi na kosa katika kanuni ya kuwekea mikono muweka mikono ni lazima awe anajua anachikifanya NAJUA MWANANGU NAJUA, HUKU AKIJUA ATIAVYO MIKONO je unajua jinsi ya kuweka mikono au unaweka tu? Sio hivyo tu jua kuwa sasa naweka mikono kwaajili ya uponyaji, au naweka mikono kwaajili ya kuchochea karama, au naweka mikono kwaajili ya kuweka kiongozi na kadhalika na wakati wote lile kusudi la kuweka mikono litatamkwa kwa maombi (kunuizia), unapoweka mikono kusimika kiongozi muwekee mkono wa kuume sio wa kushoto, shikiwa maiki na mtu kisha tumia mikono yako yute miwili muwekee mikono kiongozi mkuu, unakuta mtu ameshima maiki kwa mkono wa kulia anaweka wakfu kiongozi akitumia mkono wa kushoto na watu wote wanakodoa macho na kuona tukio hilo kama tukio la kawaida inaumiza sana watu kukosea kanuni za kuwekewa watu mikono!, Yusufu aliumia alipoona Manase anawekewa mkono wa kushoto kwa nini kwa sababu alitambua kimsingi kanuni hii

Kuweka au kuwekea mikono ni urithi wa kiroho – Katika ulimwengu wa roho tendo la kumuwekea mtu mikono ni tendo la kurithi, au kurithisha tunajifunza kuwa wakati Yakobo anaweka mikono juu ya Manase na Efraimu hawa walikuwa wajukuu wake lakini kitendo cha kuwawekea mikono kilibadilisha mfumo wa maisha ya Manase na Efraimu kutoka kuwa wajukuu zake na kuwa watoto wake sawa kabisa na Simeoni na Reuben  ona

Mwanzo 48:3-6 “Yakobo akamwambia Yusufu, Mungu Mwenyezi alinitokea huko Luzu, katika nchi ya Kanaani, akanibariki, akaniambia, Mimi hapa, nitakuongezea uzao wako, na kukuzidisha, nami nitakufanya uwe kundi la mataifa; kisha nitawapa wazao wako nchi hii baada yako, iwe milki ya milele. Basi sasa wanao wawili uliozaliwa katika nchi ya Misri kabla sijaja kwako Misri ni watoto wangu, yaani, Efraimu na Manase watakuwa wangu, kama Reubeni na Simeoni. Na wazao wako utakaozaa baada ya hawa watakuwa wako; kwa jina la ndugu zao wataitwa katika urithi wao.”

Hii maana yake ni nini anayeweka mikono anawarithi anaowawekea mikono kuwa wanaye na wanaowekewa mikono wanamrithi anayewawekea mikono kuwa baba yao nadhani ni katika dhana kama hii kumekuwa na hofu kwa watu wengi kuogopa kuwekewa mikono na kila mtu kwa kuhofia kuwa baba wa mtu ambaye humjui vema au kuwarithi watoto usiowafahamu vema kwa kuwa katika ulimwengu wa roho mnabadilishana DNA za kimamlaka na uongozi

Kuwekea mtu mikono ni kumuidhinisha au kumtambulisha – Tendo la kuwekea mtu mikono ni tendo la kumuidhinisha au kumtambulisha mtu kihuduma au kumuweka katika mamlaka ya uongozi, unamuweka mtu wakfu kwaajili ua huduma aliyoteuliwa au kuchaguliwa kuifanya kama ushemasi, umisheni na kadhalika kwa hiyo kitendo cha kumuwekea mikono ni utambuzi wa hadharani kuhusu aina ya wito aliyoitiwa anayewekea mikono au kuchochea karama au kuhamishia karama na mamlaka kumuwezesha mtu huyo kutumikia vema kusudi alilowekewa  na ndio maana bado Biblia inatoa tahadhari kuwa na umakini na unayemuwekea mikono ili kama ni mwovu kumuwekea mikono maana yake ni kushiriki kazi zake mbovu au kushiriki uovu kwa hiyo lazima unayemuwekea mikono uwe umemthibitisha kuwa hatakuaibisha

1Timotheo 5:21-22 “Nakuagiza mbele za Mungu, na mbele za Kristo Yesu, na mbele za malaika wateule, uyatende hayo pasipo kuhukumu kwa haraka; usifanye neno lo lote kwa upendeleo. Usimwekee mtu mikono kwa haraka, wala usizishiriki dhambi za watu wengine. Ujilinde nafsi yako uwe safi.”      

Unapomuwekea mtu mikono kwaajili ya huduma maana yake unagonga muhuri wako na kumuidhinisha mtu huyo katika huduma ile aliyoitiwa sasa endapo mtu huyu hayuko sawa maana yake kushindwa kwake kunawakilisha kushindwa kwako, wekea mikono mtu anayekuwakilisha vema, ambaye umemfunza vema  

Kuwekea mikono ni njia ya kupitisha neema ya Mungu.- tendo la kuwekea mikono kama ilivyo tendo la kupaka mafuta yote ni matendo ya kuipitisha neema ya Mungu kupitia mikono yetu kwenda kwa wengine kwa hiyo ni lazima tendo hili litumike pamoja na Maombi, kama ni kwaajili ya mgonjwa kutakuwa na dua maalumu kwajili ya mgonjwa kama ni kwaajili ya kuweka wakfu kiongozi dua itatamkwa ya kuweka wakfu kwa viongozi wanaohisika na waliokidhi vigezo

Yakobo 5:14-15 “Mtu wa kwenu amekuwa hawezi? Na awaite wazee wa kanisa; nao wamwombee, na kumpaka mafuta kwa jina la Bwana. Na kule kuomba kwa imani kutamwokoa mgonjwa yule, na Bwana atamwinua; hata ikiwa amefanya dhambi, atasamehewa.”

Matendo 15:40-41 “Lakini Paulo akamchagua Sila, akaondoka, akiombewa na wale ndugu apewe neema ya Bwana. Akapita katika Shamu na Kilikia akiyathibitisha makanisa.”

Kwa hiyo ibada zote za kuwekea mikono iwe ni kwaajili ya uponyaji, kubariki ndoa kuweka viongozi zote maana yake ni kuruhusu neema ya Mungu ipite juu ya wahusika na kuwawezesha katika wajibu unaohusika kwa hiyo ni lazima maombi yahusike kwa sababu hiyo kuwekea mikono sio uchawi ni njia ya kupitisha neema ya Mungu kwa hiyo kuwekea mikono ni njia inayoonekana ya kupitisha mambo yasiyoonekana ya kiungu kwenda kwa watu husika, kwa umaalumu wake kwa kanisa na ulimwengu lakini mwenye kutoa Baraka hizo ni Mungu mwenyewe, wakati wa kubariki watoto tunaweza kuwawekea mikono, wakati wa kubatiza tunaweza kumuwekea mtu mikono na kumuombea neema ya maisha ya uchaji wa Mungu na utumishi, wakati wa kuombea wagonjwa tunaweza kuwaombea wagonjwa neema ya kupokea uponyaji, wakati wa kubariki maharusi tunaweza kuwaombea maharusi neema na wakati wa kuweka wakfu viongozi mashemasi, makasisi, maaskofu na kadhalika na hata wakati wa kusimika askofu na viongozi mbalimbali ni vema wakawekewa mikono kuwaombea neema ya Mungu kisha Mungu mwenyewe atafanya kazi yake pamoja na watu wake kwa makusudi yaliyokusudiwa, kumbuka wakati wa kuwekea maharusi mikono ya Baraka weka mkono wa kuume kwa mume na mkono wa kushoto kwa mke kufanya kinyume na hayo ni kutengeneza migogoro ya kiroho na kimaongozi kwani Mungu hadhihakiwi waweka mikono lazima wajue nini wanachokifanya wakati wanaweka mikono. Ikiwa kanisa linaweka mikono kwa askofu mkuu, na askofu mkuu aliyekuwepo madarakani hayuko, askofu mkuu mteule atawekewa mikono na mtu mwenye mamlaka ya askofu mkuu aliyetsaafu au wa kanisa lingine, ama kutoka kwa wamishionari waanzilishi wa kanisa husika au mtu mwenye mamlaka ya huduma ya kitume.

Na. Rev. Innocent Samuel Kamote

Mkuu wa wajenzi mwenye Hekima

Jumapili, 1 Februari 2026

Nyota za Abrahamu!


Mwanzo 15:1-5. “Baada ya mambo hayo neno la BWANA likamjia Abramu katika njozi, likinena, Usiogope, Abramu, Mimi ni ngao yako, na thawabu yako kubwa sana. Abramu akasema, Ee Bwana MUNGU, utanipa nini, nami naenda zangu hali sina mtoto, na atakayeimiliki nyumba yangu ni huyu Eliezeri, Mdameski? Abramu akasema, Tazama, hukunipa uzao, na mtu aliyezaliwa nyumbani mwangu ndiye mrithi wangu. Nalo neno la BWANA likamjia likinena, Huyu hatakurithi, bali atakayetoka katika viuno vyako ndiye atakayekurithi. Akamleta nje, akasema, Tazama sasa mbinguni, kazihesabu nyota, kama ukiweza kuzihesabu. Akamwambia, Ndivyo utakavyokuwa uzao wako.”




Utangulizi:

Katika aya tulizosoma hapo juu, tunataarifiwa kuwa Mungu alimtembelea Abrahamu katika njozi na kumpa maneno ya kutia moyo, wakati huu Abrahamu alikuwa hana mtoto bado na umri wake ulikuwa umeenda sana na mke wake pia alikuwa mzee, na sasa anawaza kuacha urithi wake kwa Eliezeri mtumishi wake, kimsingi Abrahamu alikuwa amekata tamaa, na Mungu alikuja kumpasha habari za muhimu sana ambazo zilikuwa zinapita uwezo wa kufikiri kwake, wakati Abrahamu alikuwa anafikiri juu ya mtoto mmoja tu, Mungu alikuwa anafikiri uzao mwingi sana kama nyota za angani, Yeye alimleta Abrahamu nje na kumpa kazi ya kuzihesabu nyota na kisha alimhakikishia kuwa ndivyo utakavyokuwa uzao wake! Ahadi hii ya kipekee inazungumzia kuzidishwa kusikoweza kuhesabika, wema na kibali kikubwa sana cha Mungu kwa Abrahamu, na urithi wa kiroho usio na mipaka na hivyo kama wewe ni mtoto wa Abraham kwa ahadi na kwa imani maono haya yanaashiria kuwa wewe sio wa kawaida kama unavyoweza kudhani na Baraka za Mungu kwako hazina mipaka na kuwa hauko duniani kwa hasara, una ushawishi mkubwa na uwepo wako unachangia kitu Fulani duniani, wewe ni nuru inayong’aa gizani, umeinuliwa juu sana wewe si wa kawaida, maono haya hayaleti ujumbe wa uzao tu kwa Abrahamu bali pia yanaleta ujumbe kwetu kuwa sisi ni watoto wa namna gani katika uhusiano wetu na Mungu ona  

1Petro 2:9-10 “Bali ninyi ni mzao mteule, ukuhani wa kifalme, taifa takatifu, watu wa milki ya Mungu, mpate kuzitangaza fadhili zake yeye aliyewaita mtoke gizani mkaingie katika nuru yake ya ajabu; ninyi mliokuwa kwanza si taifa, bali sasa ni taifa la Mungu; mliokuwa hamkupata rehema, bali sasa mmepata rehema.”

Wafilipi 2:14-15. “Yatendeni mambo yote pasipo manung'uniko wala mashindano, mpate kuwa wana wa Mungu wasio na lawama, wala udanganyifu, wasio na ila kati ya kizazi chenye ukaidi, kilichopotoka; ambao kati ya hao mnaonekana kuwa kama mianga katika ulimwengu,”

Leo basi tutachukua muda wetu kujifunza kile Mungu anazungumza na Abrahamu kutuhusu sisi pamoja na wana wa Abrahamu wengineo na kile ambacho Mungu alikuwa anamaanisha katika ujumbe wake kwa Abrahamu na kwetu tutajifuza somo hili “Nyota za Abrahamu” kwa kuzingatia vipengele muhimu vitatu vifuatavyo:-


·         Maana ya Nyota za Abrahamu

·         Nyota za Abrahamu

·         Jinsi ya kuwa nyota za Abrahamu

 

Maana ya Nyota za Abrahamu.

Mwanzo 15:1-5. “Baada ya mambo hayo neno la BWANA likamjia Abramu katika njozi, likinena, Usiogope, Abramu, Mimi ni ngao yako, na thawabu yako kubwa sana. Abramu akasema, Ee Bwana MUNGU, utanipa nini, nami naenda zangu hali sina mtoto, na atakayeimiliki nyumba yangu ni huyu Eliezeri, Mdameski? Abramu akasema, Tazama, hukunipa uzao, na mtu aliyezaliwa nyumbani mwangu ndiye mrithi wangu. Nalo neno la BWANA likamjia likinena, Huyu hatakurithi, bali atakayetoka katika viuno vyako ndiye atakayekurithi. Akamleta nje, akasema, Tazama sasa mbinguni, kazihesabu nyota, kama ukiweza kuzihesabu. Akamwambia, Ndivyo utakavyokuwa uzao wako.”

Ni muhimu kufahamu kuwa asili ya ndoto hii ambayo Mungu alisema na Abrahamu ina uhusiano mkubwa na watoto wa Abrahamu wa kiroho zaidi kuliko watoto wa Abrahamu wa kimwili, kumbuka kuwa hii ilikuwa ni mara nyingine tena zaidi Mungu akizungumza na Abrahamu kuhusu uzao, hasa kwa sababu ya hali yake ya kutokuwa na watoto, Mungu alizungumza kwa namna mbili tofauti na ni lazima namna zote mbili tuzielewe vema, anapozungumza na Abrahamu kuhusu uzao mwingi na uzao wa kimwili au kibaiolojia Mungu anamwambia Abrahamu kuwa uzao wako utakuwa mwingi kama Mchanga au kama mavumbi ya nchi!

Mwanzo 13:14-18 “BWANA akamwambia Abramu, alipokwisha kutengana na Lutu, Inua sasa macho yako, ukatazame kutoka hapo ulipo, upande wa kaskazini, na wa kusini na wa mashariki na wa magharibi;maana nchi hii yote uionayo, nitakupa wewe na uzao wako hata milele.Na uzao wako nitaufanya uwe kama mavumbi ya nchi; hata mtu akiweza kuyahesabu mavumbi ya nchi, uzao wako nao utahesabika. Ondoka, ukatembee katika nchi hii katika mapana yake, na marefu yake, maana nitakupa wewe nchi hiyo. Basi Abramu akajongeza hema yake, akaja akakaa kwenye mialoni ya Mamre, nayo ni miti iliyoko Hebroni, akamjengea BWANA madhabahu huko.”

Hesabu 23:8-10 “Nimlaanije, yeye ambaye Mungu hakumlaani? Nimshutumuje, yeye ambaye Bwana hakumshutumu? Kutoka kilele cha majabali namwona; Na kutoka milimani namtazama; Angalia, ni watu wakaao peke yao, Wala hawatahesabiwa pamoja na mataifa. Ni nani awezaye kufanya idadi ya mavumbi ya Yakobo, Au kuhesabu robo ya Israeli? Na nife kifo chake mwenye haki, Na mwisho wangu uwe mfano wa mwisho wake.”     

Mwanzo 32:10-12 “mimi sistahili hata kidogo hizo rehema zote na kweli yote uliyomfanyia mtumwa wako; maana nalivuka mto huo wa Yordani na fimbo yangu tu, na sasa nimekuwa matuo mawili.Uniokoe sasa na mkono wa ndugu yangu, mkono wa Esau, maana mimi namwogopa, asije akanipiga, na mama pamoja na wana. Nawe ulisema, Hakika nitakutendea mema, nami nitafanya uzao wako uwe kama mchanga wa bahari, usiohesabika kwa kuwa mwingi.”           

Mungu anazungumza na Abrahamu katika fungu hili akumuahidi watoto wa mwilini, wale watakaoirithi nchi pale mashariki ya kati, watoto hawa wanawakilishwa na mavumbi ya nchi, mchanga au mchanga wa bahari, na hapo katika lugha za kinabii wanazungumziwa watoto wa Abrahamu wa kimwili wa kidunia  wanaweza kuwa Wayahudi na Waarabu wa kawaida wasiookoka, kwa hiyo tunafunuliwa hapa katika maandiko kuwa Abrahamu ana watoto wa aina mbili wa mwilini na watoto wa kiroho, au waliozaliwa kwa mwili na wale waliozaliwa kwa Ahadi, tunafahamu kuwa baada ya kifo cha Sara Abraham alikuwa na watoto wengine kupitia Ketura ambao ni Zimran. Yokshan, Medani, Midiani Ishbaki na Shua ambao wengi wanaunda falme za kiarabu mashariki ya kati hata hivyo Ishamel na Isaka ndio wanaotumika zaidi kitheolojia kutufunza watoto hao wa aina mbili wa Abrahamu, yaani mmoja wa mwilini na mwingine wa ahadi, mmoja wa mjakazi na mwingine wa Muungwana, sasa hawa wanawakilishwa na mavumbi na nyota, mavumbi ni wale wa mwilini na Nyota ni wale wa Rohoni, au wa ahadi.

Wagalatia 4:22-23 “Kwa maana imeandikwa ya kuwa, Ibrahimu alikuwa na wana wawili mmoja kwa mjakazi, na mmoja kwa mwungwana. Lakini yule wa mjakazi alizaliwa kwa mwili, yule wa mwungwana kwa ahadi.”

Kwa hiyo maana ya maono ya nyota za Abrahamu hapo, wanazungumziwa watoto wa kiroho wa Abrahamu wana wa ahadi, wale wanaomwamini Mungu kama Abrahamu alivyomwamini Mungu akahesabiwa kuwa na haki, hawa ni wale waliookoka waliomwamini Yesu kama Bwana na mwokozi kutoka kila mahali duniani wawe ni Wayahudi au Wayunani vyovyote kama wamemuamini Bwana Yesu kwa imani hao ni wana wa Ibrahimu wanaotajwa kama nyota

Wagalatia 3:6-9 “Kama vile Ibrahimu alivyomwamini Mungu akahesabiwa haki.Fahamuni basi, ya kuwa wale walio wa imani, hao ndio wana wa Ibrahimu.Na andiko, kwa vile lilivyoona tangu zamani kwamba Mungu atawahesabia haki Mataifa kwa imani, lilimhubiri Ibrahimu habari njema zamani, kusema, Katika wewe Mataifa yote watabarikiwa. Basi hao walio wa imani hubarikiwa pamoja na Ibrahimu aliyekuwa mwenye imani.”

Kwa hiyo Mungu anapozungumza na Abrahamu kwa habari ya watoto wa Mwilini anamuahidi uzao kama mavumbi ya nchi na anapozungumza naye kuhusu watoto wa kiroho anazungumza na Abrahamu kwa ahadi ya kuhesabia nyota, kwa hiyo nyota za Abrahamu ni watoto wake wa kiroho yaani wewe na mimi tuliookoka tulio mwamini Yesu na kuhesabiwa haki kwa imani sisi ndio “Nyota za Abrahamu” kwa hiyo katika ahadi ya uzao kwa Ibrahimu kumbuka kuna uzao kama nyota za angani na uzao kama mchanga wa bahari au mavumbi ya nchi hii inatofautisha watoto wa mwilini na watoto wa rohoni  wa Ibrahimu mwenye kusikia na asikie! Mungu anaahidi kuwabariki watoto hao wote

Mwanzo 22:16-18. “akasema, Nimeapa kwa nafsi yangu asema BWANA, kwa kuwa umetenda neno hili, wala hukunizuilia mwanao, mwanao wa pekee, katika kubariki nitakubariki, na katika kuzidisha nitauzidisha uzao wako KAMA NYOTA ZA MBINGUNI, na KAMA MCHANGA ULIOKO PWANI; na uzao wako utamiliki mlango wa adui zao; na katika uzao wako mataifa yote ya dunia watajibarikia; kwa sababu umetii sauti yangu.”

Nyota za Abrahamu.

Mwanzo 15:1-5. “Baada ya mambo hayo neno la BWANA likamjia Abramu katika njozi, likinena, Usiogope, Abramu, Mimi ni ngao yako, na thawabu yako kubwa sana. Abramu akasema, Ee Bwana MUNGU, utanipa nini, nami naenda zangu hali sina mtoto, na atakayeimiliki nyumba yangu ni huyu Eliezeri, Mdameski? Abramu akasema, Tazama, hukunipa uzao, na mtu aliyezaliwa nyumbani mwangu ndiye mrithi wangu. Nalo neno la BWANA likamjia likinena, Huyu hatakurithi, bali atakayetoka katika viuno vyako ndiye atakayekurithi. Akamleta nje, akasema, Tazama sasa mbinguni, kazihesabu nyota, kama ukiweza kuzihesabu. Akamwambia, Ndivyo utakavyokuwa uzao wako.”

Kimsingi katika maono haya Mungu alikuwa anafanya agano na Abrahamu kuwa atakuwa na watoto wa agano au watoto wa ahadi, au watoto wa imani ambao watakuwa na uwezo mkubwa sana na wenye Baraka za kudumu, watakuwa ni watoto ambao hawawezi kueleweka kwa hesabu za kibinadamu, watakuwa na ushawishi mkubwa duniani, watatoa muelekeo, wataipa dunia nuru, watatofautishwa na giza, wao hawatakuwa wa kawaida, wasioweza kuwekewa mipaka, wasiohesabika, watoto hao ni sisi na uweza wao unaelezewa katika maandiko kwa njia ya kipeke

1.       Ni watoto wa Imani – Abrahamu alikuwa katika mashaka makubwa sana , umri unaenda mkewe amezeeka na anawasiwasi kuhusu warithi wake, Lakini kwa Mungu hiyo haikuwa shida alikuwa amekusudia kumpa Abrahamu watoto wa aina zote watoto wa mwilini na watoto wa rohoni na wote wangekuwa wengi sana wa mwilini kama mchanga wa bahari na wa kiroho au wa Imani kama nyota  za mbinguni ona:-

 

Mwanzo 22:16-18. “akasema, Nimeapa kwa nafsi yangu asema BWANA, kwa kuwa umetenda neno hili, wala hukunizuilia mwanao, mwanao wa pekee,katika kubariki nitakubariki, na katika kuzidisha nitauzidisha uzao wako KAMA NYOTA ZA MBINGUNI, na KAMA MCHANGA ULIOKO PWANI; na uzao wako utamiliki mlango wa adui zao; na katika uzao wako mataifa yote ya dunia watajibarikia; kwa sababu umetii sauti yangu.”

 

Watoto wanaofananishwa na Nyota za mbinguni ni watoto wa kiroho ni watoto wa Imani, hawa sio wale wanaozaliwa kwa damu na nyama bali ni wale wanaozaliwa kwa imani wale waliomwamini Mungu kama Ibrahimu aliyomwamini Mungu na kuhesabiwa kuwa haki.

 

Wagalatia 3:6-9 “Kama vile Ibrahimu alivyomwamini Mungu akahesabiwa haki.Fahamuni basi, ya kuwa wale walio wa imani, hao ndio wana wa Ibrahimu.Na andiko, kwa vile lilivyoona tangu zamani kwamba Mungu atawahesabia haki Mataifa kwa imani, lilimhubiri Ibrahimu habari njema zamani, kusema, Katika wewe Mataifa yote watabarikiwa.Basi hao walio wa imani hubarikiwa pamoja na Ibrahimu aliyekuwa mwenye imani.”

 

2.       Ni watoto wasio na mipaka - Akamleta nje, akasema, Tazama sasa mbinguni, kazihesabu nyota, kama ukiweza kuzihesabu. Akamwambia, Ndivyo utakavyokuwa uzao wako, Mungu alimtoa Abrahamu nje, ilikuwa nje ya hema yake, ilikuwa nje ya kuta za nyumba, ilikuwa nje ya dunia,  ilikuwa nje ya mipaka ya kimazingira, ilikuwa nje ya fikra finyu, inayoishia kwenye anga la dunia, akamwangalisha juu, alimtazamisha mbinguni akamuamuru ahesabie nyota kama ataweza akamwambia ndivyo utakavyokuwa uzao wako, Mungu alikuwa anasema na Abrahamu kuwa wazao wake Nyota za Abrahamu hawatakuwa na mipaka, wala hawawezi kuhesabiwa kwa hesabu za kidunia wala za kibinadamu, mtu yeyote anayetaka kuangalia mambo kwa upana haangalii mambo ya duniani pekee, anaangalia yaliyo juu, watoto wa Abrahamu au nyota za Abrahamu huangalia mambo kwa upana, wanaona mbali, hawaangalii vya muda wanaaangalia vya milele, hawafikri yaliyo katika nchi pekee wanafikiri yaliyo juu, huwezi kuwawekea mipaka watu wenye mtazamo unaozidi mtazamo wa kidunia, nyota hazikai katika anga hili nyota zinakaa mbali ziko juu sana na ni kubwa mno

 

Wakolosai 3:1-2 “Basi mkiwa mmefufuliwa pamoja na Kristo, yatafuteni yaliyo juu Kristo aliko, ameketi mkono wa kuume wa Mungu. Yafikirini yaliyo juu, siyo yaliyo katika nchi.”

 

2Wakorintho 4:16-18. “Kwa hiyo hatulegei; bali ijapokuwa utu wetu wa nje unachakaa, lakini utu wetu wa ndani unafanywa upya siku kwa siku. Maana dhiki yetu nyepesi, iliyo ya muda wa kitambo tu, yatufanyia utukufu wa milele uzidio kuwa mwingi sana; tusiviangalie vinavyoonekana, bali visivyoonekana. Kwa maana vinavyoonekana ni vya muda tu; bali visivyoonekana ni vya milele.

 

3.       Ni watoto wenye wito wa mbinguni – Nyota za Abrahamu ni watoto wa Imani wa Ibrahimu ambao wameitwa na Mungu kwaajili ya wito mkuu wa Mungu wa maisha yasiyokuwa ya kawaida kusudi lao si la kidunia kusudi lao ni la kimbingu, ni watu ambao wenyeji wao uko mbinguni wao wako ulimwenguni lakini sio wa ulimwengu huu,  

 

Waebrania 3:1-2. “Kwa hiyo, ndugu watakatifu, wenye kuushiriki mwito wa mbinguni, mtafakarini sana Mtume na Kuhani Mkuu wa maungamo yetu, Yesu, aliyekuwa mwaminifu kwake yeye aliyemweka, kama Musa naye alivyokuwa, katika nyumba yote ya Mungu.”

 

Wafilipi 3:20-21 “Kwa maana sisi, wenyeji wetu uko mbinguni; kutoka huko tena tunamtazamia Mwokozi, Bwana Yesu Kristo; atakayeubadili mwili wetu wa unyonge, upate kufanana na mwili wake wa utukufu, kwa uweza ule ambao kwa huo aweza hata kuvitiisha vitu vyote viwe chini yake.”

 

Yohana 15:18-19. “Iwapo ulimwengu ukiwachukia, mwajua ya kuwa umenichukia mimi kabla ya kuwachukia ninyi. Kama mngekuwa wa ulimwengu, ulimwengu ungewapenda walio wake; lakini kwa kuwa ninyi si wa ulimwengu, bali mimi naliwachagua katika ulimwengu, kwa sababu hiyo ulimwengu huwachukia.”

 

4.       Ni watoto wenye hekima isiyo ya dunia hii – Watoto wa Abrahamu au nyota za Abrahamu ni wenye kutoa muongozo. Wanatoa nuru na wako tofauti na wana wa giza, tofauti na wana siasa na watawala wa dunia hii hekima waliyonayo wanaitumia kuwavuta wengi na kuwaongoza katika kuishi maisha ya haki, Nyota zinaashiria ushawishi wenye manufaa, zinaashiria uwezo wa juu wa kimtazamo, mawazo  mapana na hekima ya hali ya juu, hekima isiyokuwa ya kawaida, isiyo ya duania hii, hekima iliyohifadhiwa kwaajili yetu tu

 

Daniel 12:3 “Na walio na hekima watang'aa kama mwangaza wa anga; na hao waongozao wengi kutenda haki watang'aa kama nyota milele na milele.”

 

1Wakorintho 2:6-7 “Walakini iko hekima tusemayo kati ya wakamilifu; ila si hekima ya dunia hii, wala ya hao wanaoitawala dunia hii, wanaobatilika; bali twanena hekima ya Mungu katika siri, ile hekima iliyofichwa, ambayo Mungu aliiazimu tangu milele, kwa utukufu wetu;

 

Yakobo 3:15-17 “Hekima hiyo siyo ile ishukayo kutoka juu, bali ni ya dunia, ya tabia ya kibinadamu, na Shetani. Maana hapo palipo wivu na ugomvi ndipo palipo machafuko, na kila tendo baya. Lakini hekima itokayo juu, kwanza ni safi, tena ni ya amani, ya upole, tayari kusikiliza maneno ya watu, imejaa rehema na matunda mema, haina fitina, haina unafiki.”

 

5.       Ni watoto wa Nuru – Nyota zina sifa maalumu na sifa mojawapo ni kung’aa gizani, na hivyo kuziwezesha kung’aa usiku zadi wakati dunia ikiwa giza, dunia inapokuwa imeharibiwa na giza la dhambi, giza la kutokuyajua mapenzi ya Mungu, giza la kutokuona mbele, giza la kutokumfahamu Mungu watoto wa Abrahamu ambao ni nyota huiangaza Dunia hawa ni wana wa Nuru na kamwe sio wana wa giza, kazi yao ni kuleta ufumbuzi, ni kuiangazia dunia isiwe na ukiwa, isiwe na giza, isipoteze ladha  na isiwe yenye kutisha

 

Mathayo 5:14-16 “Ninyi ni nuru ya ulimwengu. Mji hauwezi kusitirika ukiwa juu ya mlima. Wala watu hawawashi taa na kuiweka chini ya pishi, bali juu ya kiango; nayo yawaangaza wote waliomo nyumbani.Vivyo hivyo nuru yenu na iangaze mbele ya watu, wapate kuyaona matendo yenu mema, wamtukuze Baba yenu aliye mbinguni.”

 

1Wathesalonike 5:4-5 “Bali ninyi, ndugu, hammo gizani, hata siku ile iwapate kama mwivi. Kwa kuwa ninyi nyote mmekuwa wana wa nuru, na wana wa mchana; sisi si wa usiku, wala wa giza.”

       

6.       Ni watoto wenye uwezo wa kutangaza fadhili/utukufu wa Mungu – Nyota za Abrahamu maisha yao ni ya ushindi na ushuhuda, tabia zao na matendo yao humtukuza Mungu, na shuhuda zao zinatangaza fadhili za Mungu, Kama jinsi maandiko yasemavyo kuwa moja ya kazi za anga au mbingu ni kuhubiri utukufu wa Mungu hivyo ndivyo uzao wa Abrahamu yaani nyota za Abrahamu hutangaza fadhili na utukufu wa Mungu

 

Zaburi 19:1-4 “Mbingu zauhubiri utukufu wa Mungu, Na anga laitangaza kazi ya mikono yake. Mchana husemezana na mchana, Usiku hutolea usiku maarifa.Hakuna lugha wala maneno, Sauti yao haisikilikani. Sauti yao imeenea duniani mwote, Na maneno yao hata miisho ya ulimwengu. Katika hizo ameliwekea jua hema,”

 

1Petro 2:9-10 “Bali ninyi ni mzao mteule, ukuhani wa kifalme, taifa takatifu, watu wa milki ya Mungu, mpate kuzitangaza fadhili zake yeye aliyewaita mtoke gizani mkaingie katika nuru yake ya ajabu; ninyi mliokuwa kwanza si taifa, bali sasa ni taifa la Mungu; mliokuwa hamkupata rehema, bali sasa mmepata rehema.”

 

7.       Ni watoto wasioweza kurogeka wala kulaanika – Nyota za Abrahamu ni watoto waliobarikiwa ambao nguvu za giza, uchawi na waganga hauwawezi, wao wanalindwa na nguvu za Mungu awaye yote atakayejaribu kufanya lolote la kichawi au la kiganga kwa lengo la kuwadhuru watoto wa Abrahamu wa Imani atashughulikiwa na Mungu mwenyewe. Watoto wa duniani wanaweza kurogwa kwa kuchukua Mchanga wa mbinguni utachukua nini huwezo kuchota nyao za watoto wa mbinguni, huwezi kufukia kitu kwao ukatoboa hawarogeki!

 

Hesabu 23:7-9 “Akatunga mithali yake, akasema, Balaki amenileta kutoka Aramu, Mfalme wa Moabu kutoka milima ya mashariki, Njoo! Unilaanie Yakobo, Njoo! Unishutumie Israeli. Nimlaanije, yeye ambaye Mungu hakumlaani? Nimshutumuje, yeye ambaye Bwana hakumshutumu? Kutoka kilele cha majabali namwona; Na kutoka milimani namtazama; Angalia, ni watu wakaao peke yao, Wala hawatahesabiwa pamoja na mataifa.”

 

Hesabu 23:18-24 “Naye akatunga mithali yake, akasema, Ondoka Balaki, ukasikilize; Nisikilize, Ee mwana wa Sipori; Mungu si mtu, aseme uongo; Wala si mwanadamu, ajute; Iwapo amesema, hatalitenda? Iwapo amenena, hatalifikiliza? Tazama, nimepewa amri kubariki, Yeye amebariki, nami siwezi kulitangua. Hakutazama uovu katika Yakobo, Wala hakuona ukaidi katika Israeli. Bwana, Mungu wake, yu pamoja naye, Na sauti kuu ya mfalme i katikati yao. Mungu amewaleta kutoka Misri, Naye ana nguvu kama nguvu za nyati. Hakika hapana uchawi juu ya Yakobo, Wala hapana uganga juu ya Israeli. Sasa habari za Yakobo na Israeli zitasemwa, Ni mambo gani aliyoyatenda Mungu! Tazama, watu hawa wanaondoka kama simba mke, Na kama simba anajiinua nafsi yake, Hatalala hata atakapokula mawindo, Na kunywa damu yao waliouawa.”

 

8.       Watawashinda adui zao – Hakuna adui atakayeweza kusimama kinyume na Nyota za Abrahamu, Neno la Mungu la kinabii limeahidi ushindi dhidi ya adui wote wanaowazunguka watoto wa Abrahamu, watakata pembe za adui zao, watawavunja vunja wana wote wa ghasia, Uzao huu utamiliki mlango wa adui zao

 

Hesabu 24:16-19 “Asema, yeye asikiaye maneno ya Mungu, Na kuyajua maarifa yake Aliye Juu. Yeye aonaye maono ya Mwenyezi, Akianguka kifudifudi, amefumbuliwa macho, Namwona, lakini si sasa; Namtazama, lakini si karibu; Nyota itatokea katika Yakobo Na fimbo ya enzi itainuka katika Israeli; Nayo itazipiga-piga pembe za Moabu, Na kuwavunja-vunja wana wote wa ghasia. Na Edomu itakuwa milki Seiri pia itakuwa milki, waliokuwa adui zake; Israeli watakapotenda kwa ushujaa.Mwenye kutawala atakuja toka Yakobo, Atawaangamiza watakaobaki mjini.”

Mwanzo 22:16-18. “akasema, Nimeapa kwa nafsi yangu asema BWANA, kwa kuwa umetenda neno hili, wala hukunizuilia mwanao, mwanao wa pekee, katika kubariki nitakubariki, na katika kuzidisha nitauzidisha uzao wako KAMA NYOTA ZA MBINGUNI, na KAMA MCHANGA ULIOKO PWANI; na uzao wako utamiliki mlango wa adui zao; na katika uzao wako mataifa yote ya dunia watajibarikia; kwa sababu umetii sauti yangu.”

                                 

Jinsi ya kuwa nyota za Abrahamu

Ni muhimu kuwa na uelewa na ufahamu kuwa Nyota za Abrahamu sio swala la ndoto na maono ya kawaida Nyota za Abrahamu leo ni mimi na wewe, Nyota za Abrahamu ni wana wa angani ni wana wa ahadi, Abrahamu ana wana wa aina mbili Nyota na Vumbi, wewe mwenyewe unaweza kuchagua kuwa mwana wa Abrahamu kwa maisha yako unaishije? Unaangaza au umefichwa, umefufuka au umezikwa, ni wa chini au ni wa juu wewe ni wa ulimwengu huu au wewe sio wa ulimwengu huu, wewe ni mwana wa Nuru au u mwana wa giza  unaishi kwa Imani au kwa kuona? una mchango duniani kwa kuangaza au huangazi, kama wewe ni mwana wa Abrahamu Nyota za Abrahamu utaenenda kwa Imani na sio kwa kuona, pale ambapo dunia inasema haiwezekani watu wa Mungu wanasema inawezekana, wana wa Abrahamu ni watoto wenye Imani, wanaishi wakimpendeza Mungu kwa Imani, hakuna jambo lenye mipaka Mbinguni, wakiroga mavumbi ya ardhi sisi haturogeki mpaka upande mbinguni, ukituweka kwenye giza tunang’aa,. Sisi ni wana wa ahadi ahatukuzaliwa kwa mwili, sisi ni wa maono ya kimbinguni na sio ya kidunia huwezi kumuwekea mipaka kwa uhuru tulio nao angani, unataka kuwa mwana wa Abrahamu ambaye ni Nyota hapa duniani uokoke leo, unataka kuwa Mwana wa Abrahamu mavumbi usiokoke ukanywagwe duniani.

2Wakorintho 5:7-9 “(Maana twaenenda kwa imani, si kwa kuona.) Lakini tuna moyo mkuu; nasi tunaona ni afadhali kutokuwamo katika mwili na kukaa pamoja na Bwana. Kwa hiyo, tena, ikiwa tupo hapa, au ikiwa hatupo hapa, twajitahidi kumpendeza yeye

Luka 19:8-10 “Zakayo akasimama, akamwambia Bwana, Tazama, Bwana, nusu ya mali yangu nawapa maskini, na ikiwa nimenyang'anya mtu kitu kwa hila namrudishia mara nne.Yesu akamwambia, Leo wokovu umefika nyumbani humu, kwa sababu huyu naye ni mwana wa Ibrahimu. Kwa kuwa Mwana wa Adamu alikuja kutafuta na kuokoa kile kilichopotea.”

Zakayo alikuwa Myahudi, lakini alikuwa uzao wa Abrahamu upande wa mavumbi, lakini alipookolewa Yesu alisema huyu naye ni mwana wa Ibrahimu, ukimkubali Yesu kuanzia leo unakuwa mwana wa Ibrahimu, ukiendelea kung’ang’ania dini kama mafarisayo unapoteza sifa ya kuwa mwana wa Ibrahimu, Wayahudi wengi waligeuka kuwa wana wa Ibilisi na wana wa mavumbi na kamwe hawakuwa nyota ya Abrahamu kwa sababu dini iliwageuza wakawa na roho mbaya na wauaji, wenye kujihesabia haki na wala hawakutenda mapenzi ya Mungu unataka kuwa Nyota za Abrahamu toka gizani leo uje nuruni, Mwombe Mungu uokolewe! Ukiokoka na kumwamini Yesu wewe ni nyota!

Yohana 8:39-44 “Wakajibu, wakamwambia, Baba yetu ndiye Ibrahimu! Yesu akawaambia, Kama mngekuwa watoto wa Ibrahimu, mngezitenda kazi zake Ibrahimu.Lakini sasa mnatafuta kuniua mimi, mtu ambaye nimewaambia iliyo kweli, niliyoisikia kwa Mungu. Ibrahimu hakufanya hivyo. Ninyi mnazitenda kazi za baba yenu. Ndipo walipomwambia, Sisi hatukuzaliwa kwa zinaa; sisi tunaye Baba mmoja, yaani, Mungu. Yesu akawaambia, Kama Mungu angekuwa baba yenu, mngenipenda mimi; kwa maana nalitoka kwa Mungu, nami nimekuja; wala sikuja kwa nafsi yangu, bali yeye ndiye aliyenituma. Mbona hamyafahamu hayo niyasemayo? Ni kwa sababu ninyi hamwezi kulisikia neno langu. Ninyi ni wa baba yenu, Ibilisi, na tamaa za baba yenu ndizo mpendazo kuzitenda. Yeye alikuwa mwuaji tangu mwanzo; wala hakusimama katika kweli, kwa kuwa hamna hiyo kweli ndani yake. Asemapo uongo, husema yaliyo yake mwenyewe; kwa sababu yeye ni mwongo, na baba wa huo.”

Wafilipi 2:14-15. “Yatendeni mambo yote pasipo manung'uniko wala mashindano, mpate kuwa wana wa Mungu wasio na lawama, wala udanganyifu, wasio na ila kati ya kizazi chenye ukaidi, kilichopotoka; ambao kati ya hao mnaonekana kuwa kama mianga katika ulimwengu,”

Rev. Innocent Samuel Kamote

Mkuu wa wajenzi mwenye Hekima!