Jumanne, 14 Julai 2026

Nafsi yangu kwa nini kuinama?


Zaburi 42:5-6 “Nafsi yangu, kwa nini kuinama, Na kufadhaika ndani yangu? Umtumaini Mungu; Kwa maana nitakuja kumsifu, Aliye afya ya uso wangu, Na Mungu wangu. Nafsi yangu imeinama ndani yangu, kwa hiyo nitakukumbuka, Toka nchi ya Yordani, na Mahermoni, na toka kilima cha Mizari.”



Utangulizi:

Ni muhimu kufahamu kuwa ziko nyakati katika maisha ya mwanadamu na hata watu wa Mungu ambapo tunapitia vipindi ambavyo nasfi zetu zinainama kwa sababu ya kuzidiwa na maumivu ya  kihisia na kiroho, kunakosababishwa na huzuni, kukata tamaa, kukosa utulivu, kuwa na mashaka kusongwa na mawazo, hofu, kutokujitosheleza. Misiba na kuwa mbali na nyumbani au kuwa  ugenini au uhamishoni, Watakatifu waliotutangulia wanaonyesha kuwa nao pia katika nyakati tofauti tofauti walipitia hali hizi za kuzidiwa na mgandamizo wa mawazo, kukosa tumaini, kuhisi kama Mungu yuko mbali nao na kuelemewa na changamoto za maisha na upweke na hivyo kusababisha nafsi zao kuinama. Kutokana na hali hizo wakati mwingine waliziuliza nafsi zao maswali makali kwanini nafsi yangu unainama ilihali Mungu yupo? Kwa nini kufadhaika? Wakati Mungu ni tumaini lako?  Ona;-

Zaburi 43:3-5 “Niletewe nuru yako na kweli yako ziniongoze, Zinifikishe kwenye mlima wako mtakatifu na hata maskani yako. Hivyo nitakwenda madhabahuni kwa Mungu, kwa Mungu aliye furaha yangu na shangwe yangu; Nitakusifu kwa kinubi, Ee MUNGU, Mungu wangu. Nafsi yangu, kwa nini kuinama, Na kufadhaika ndani yangu? Umtumaini Mungu; Kwa maana nitakuja kumsifu, Aliye afya ya uso wangu, Na Mungu wangu.”

Nafsi zetu zinaweza kuinama sio kwa sababu ya changamoto za maisha pekee lakini pia wakati mwingine ile hali ya maumivu ya kihisia, kiu ya kuhitaji uwepo wa Mungu, ukavu wa kiroho na ile tamaa ya kutaka uwepo wa Mungu uwe ndani yetu kwa wingi ili tuweze kuzishinda changamoto za nje kwa hiyo tunajifunza hapo kuwa tunaweza kuzihubiri nafsi zetu kuzikemea, kusema nazo na kuzitaka nafsi zetu zisivunjike moyo wala zisifadhaike na badala yake zimtegemee Mungu. tutajifunza somo hili Nafsi yangu kwa nini kuinama kwa kuzingatia vipengele vitatu muhimu vifuatavyo:-

·         Maana ya nafsi kuinama.

·         Sababu zinazopelekea nafsi zetu kuinama.

·         Nafsi yangu kwa nini kuinama?


Maana ya nafsi kuinama

Zaburi 42:5-6 “Nafsi yangu, kwa nini kuinama, Na kufadhaika ndani yangu? Umtumaini Mungu; Kwa maana nitakuja kumsifu, Aliye afya ya uso wangu, Na Mungu wangu. Nafsi yangu imeinama ndani yangu, kwa hiyo nitakukumbuka, Toka nchi ya Yordani, na Mahermoni, na toka kilima cha Mizari.”

Ni muhimu kufahamu kuwa neno nafsi iliyoinama katika lugha ya Kiebrania inasomeka kama “Shachach Nephesh” misamiati ambayo kwa Kiingereza inasomeka kama “downcast soul”, “discouraged soul”, “Depressed within me” au “overwhelmed soul” maana zake kwa Kiswahili ni nasfi iliyovunjika, nafsi iliyokata tamaa, au nafsi iliyolemewa na mawazo, nafsi iliyopoteza tumaini au nafsi iliyozidiwa na kuelemewa au nafsi inayopoteza nguvu na ujasiri, nasfi ya mtu ikiinama ni ukweli ulio wazi kuwa nguvu zote zinaisha na unapoteza kiu na shauku ya kufanya lolote, mtu mwenye nasfi iliyoinama anakuwa na changamoto ya kihisia kimwili na kiroho na wakati mwingine inachangiwa na kutoweka au kupotea kwa matarajio, kutokujibiwa maombi, mambo kutokuenda sawa na kuwa na hisia kana kwamba Mungu yuko mbali, upweke wa kiroho, na kadhalika, kwa ujumla mwandishi anaonyesha kuwa nafsi yake  imeinama kwa sababu ya kuwa mbali na uwepo wa Mungu, Yeye anaonekana kuwa mbali na nyumbani, na tena mbali na Nyumba ya Mungu iliyokuwako Yerusalem, Yeye yu katika chanzo cha mto Jordani katikati ya mlima Hermoni, mahali paitwapo Mizari mbali na Hekalu la Mungu wa Israel au ukuta ule wa kulia machozi mahali pa ibada.

Sababu zinazopelekea nafsi zetu kuinama.

Kiu na hisia za kuwa mbali na Mungu – Mwanadamu mwenye akili timamu anayempenda Mungu anapokuwa na hisia za kuwa mbali na Mungu au kukosa utoshelevu wa kiibada kwa kweli anakosa amani na kuhisi kupungukiwa, Mwandishi wa Zaburi hii nyakati za agano la kale  alikuwa mbali na nyumba ya Bwana alikuwa katika sehemu ya chanzo cha mto Jordani mahali unapoishia mlima Hermoni kaskazini mwa nchi ya Israel na kuanzia kilele cha Mizari,  akiwa huko safarini mbali na nyumba ya Mungu anahisi upweke na anaona kama Mungu amemuacha, nasfi yake inaumia, mambo hayaendi na ni kama maombi yanaonekana kutokujibiwa na anakata tamaa nafsi yake inainama kwa sababu ana kiu na hisia ya kuwa mbali na Mungu  kuna namna anakosa muunganiko na Mungu wake

Zaburi 42:8-11 “Mchana Bwana ataagiza fadhili zake, na usiku wimbo wake utakuwa nami, Naam, maombi kwa Mungu aliye uhai wangu. Nitamwambia Mungu, mwamba wangu, Kwa nini umenisahau? Kwa nini ninakwenda nikihuzunika, adui wakinionea? Watesi wangu hunitukana mithili ya kuniponda mifupa yangu, Pindi wanaponiambia mchana kutwa,Yuko wapi Mungu wako? Nafsi yangu, kwa nini kuinama, Na kufadhaika ndani yangu? Umtumaini Mungu; Kwa maana nitakuja kumsifu, Aliye afya ya uso wangu, Na Mungu wangu.”

Mazingira magumu ya maisha – Mwandishi akiwa mbali na nyumba ya Mungu iliyokuwako Yerusalem anazungukwa na changamoto za maisha na mazingira magumu, anaomba kwa kulia machozi, lakini ni kama hajibiwi, huku akishutumiwa na kuhojiwa yuko wapi Mungu wake, anaonewa, anatukanwa maumivu yanaingia mpaka kwenye mifupa yake, nafsi yake inajikuta inainama, Tunapozungukwa na shida za kifamilia, ugumu wa maisha, magonjwa na kukosa mahitaji muhimu na kila aina ya fadhaa haya yote yanaweza kuisababisha nafsi ya mwanadamu kuinama.

Zaburi 42:3-5 “Machozi yangu yamekuwa chakula changu mchana na usiku, Pindi wanaponiambia mchana kutwa, Yuko wapi Mungu wako. Nayakumbuka hayo nikiweka wazi nafsi yangu ndani yangu, Jinsi nilivyokuwa nikienda na mkutano, Na kuwaongoza nyumbani kwa Mungu, Kwa sauti ya furaha na kusifu, mkutano wa sikukuu. Nafsi yangu, kwa nini kuinama, Na kufadhaika ndani yangu? Umtumaini Mungu; Kwa maana nitakuja kumsifu, Aliye afya ya uso wangu, Na Mungu wangu.”

Shinikizo kutoka kwa watu – tunaishi katika dunia ambayo wakati mwingine watu wanaweza kukuchukia bila sababu, wanasema maneno mabaya dhidi yako au wanakuzushia, au unakuwa wimbo kwenye vinywa vyao, unakataliwa, unadharauliwa, unasemwa na kusengenywa kila mahali, maneno ya watu yanakuvunja moyo unasikia jinsi wanavyokushutumu na kukusimanga na kukusema vibaya inasababisha shinikizo la maisha na kumvunja vunja mtu wa ndani na nasfi inainama

Zaburi 42:10-11 “Watesi wangu hunitukana mithili ya kuniponda mifupa yangu, Pindi wanaponiambia mchana kutwa, Yuko wapi Mungu wako? Nafsi yangu, kwa nini kuinama, Na kufadhaika ndani yangu? Umtumaini Mungu; Kwa maana nitakuja kumsifu, Aliye afya ya uso wangu, Na Mungu wangu.”

Kukumbuka nyakati nzuri zilizopita – Kuna nyakati ambapo tunakumbuka nyakati nzuri tulizokuwa nazo, nyakati za furaha na vicheko, nyakati za amani na furaha ya moyo, nyakati  huru, Mwandishi ni kama anakumbuka nyakati hizo, alikuwa anaenda Hekaluni tena akiwa kiongozi wa ibada ulikuwa ni wakati wa furaha lakini sasa wakati huo anaukosa, unaweza kukumbuka nyakati ambazo ulikuwa uko vizuri, ukilinganisha na hali ya sasa, mambo yako yalikuwa mazuri, ujana wako ulikuwa bomba na ni kama nyakati hizo zimepita haraka unakosa yale uliyokuwa ukiyatamani  na nafsi yako inainama

Zaburi 42:4-5 “Nayakumbuka hayo nikiweka wazi nafsi yangu ndani yangu, Jinsi nilivyokuwa nikienda na mkutano, Na kuwaongoza nyumbani kwa Mungu, Kwa sauti ya furaha na kusifu, mkutano wa sikukuu. Nafsi yangu, kwa nini kuinama, Na kufadhaika ndani yangu? Umtumaini Mungu; Kwa maana nitakuja kumsifu, Aliye afya ya uso wangu, Na Mungu wangu.”

Hali ya uchovu wa kiroho – Ziko nyakati ambapo kimsingi mambo yanapokuwa hayaendi uko mpweke unachoka sana unachoka kuomba, unachoka kusubiri na unaweza kuchoka hata kupigana vita nafsi inashuka na unamuhitaji Mungu, nafsi inakosa nguvu na ni mpaka Bwana akutegemeze na kukuinua kutoka hapo ulipoinama ndipo unapoweza kupenya  mwandishi alikuwa anapitia hali  hii.

Zaburi 145:13-14 “Ufalme wako ni ufalme wa zamani zote, Na mamlaka yako ni ya vizazi vyote. Bwana huwategemeza wote waangukao, Huwainua wote walioinama chini.”

Nafsi yangu kwa nini kuinama?

Mwandishi wa zaburi hii hakubaliani na hali anayoipitia na badala yake anaihoji nafsi yake kwanini kuinama? Kwanini upate shida, kwanini uteseke? Kwanini ufadhaike, yeye anaamini ya kuwa atamsifu Mungu aliye afya ya uso wake, yaani uso wake hautakuja kukunjamana kamwe, yeye ataendelea kufurahia uzuri wa Bwana kwani anaziona njia za huzuni kuwa ni swala la Muda tu  na anajua ya kuwa, Mungu huwa hakai kimya wakati nafsi zetu zinapoinama, yeye kama baba anayejali huwahurumia wamchao na kuwaokoa, Neno la Mungu linaonyesha wazi kuwa Mungu hutoa faraja ya kipekee pale watu wake wanapochoka na kuelemewa kwa hivyo badala ya kufikiri kuwa uko peke yako Neno la Mungu linaonyesha kuwa yeye atajitokeza na kutoa msaada hivyo lazima uikumbushe nafsi yako wajibu wake kwa Bwana na neno la Mungu linasema nini kukuhusu au kuihusu ili usiiname unapoikumbusha nafsi yako kuendelea kumtegema Bwana haitokuja itokee ukazimia kupitiliza:-

1.       Anaalika wote waliochoka wanaolemewa wamjie na kuwa atawapa pumziko na raha nafsini mwao. - Mathayo 11:28-30 “Njoni kwangu, ninyi nyote msumbukao na wenye kulemewa na mizigo, nami nitawapumzisha. Jitieni nira yangu, mjifunze kwangu; kwa kuwa mimi ni mpole na mnyenyekevu wa moyo; nanyi mtapata raha nafsini mwenu; kwa maana nira yangu ni laini, na mzigo wangu ni mwepesi.”

 

2.       Mungu huwapa nguvu wale waliochoka wale wanaomtumaini kama ilivyokuwa kwa mwandishi wa Zaburi hii - Isaya 40:29-31 “Huwapa nguvu wazimiao, humwongezea nguvu yeye asiyekuwa na uwezo. Hata vijana watazimia na kuchoka, na wanaume vijana wataanguka; bali wao wamngojeao Bwana watapata nguvu mpya; watapanda juu kwa mbawa kama tai; watapiga mbio, wala hawatachoka; watakwenda kwa miguu, wala hawatazimia.”

 

3.       Tunaweza kumuomba Mungu atutie nguvu pale nafsi zetu zinapochoka na kuelemewa - Zaburi 119:25-28 “Nafsi yangu imeambatana na mavumbi, Unihuishe sawasawa na neno lako. Nalizisimulia njia zangu ukanijibu, Unifundishe amri zako. Unifahamishe njia ya mausia yako, Nami nitayatafakari maajabu yako. Nafsi yangu imeyeyuka kwa uzito, Unitie nguvu sawasawa na neno lako.”

 

4.       Iambie nafsi yako imsubiri Bwana kwa kimya maana yeye hatakuangusha - Zaburi 62:1-6 “Nafsi yangu yamngoja Mungu peke yake kwa kimya, Wokovu wangu hutoka kwake. Yeye tu ndiye mwamba wangu na wokovu wangu, Ngome yangu, sitatikisika sana. Hata lini mtamshambulia mtu, Mpate kumwua ninyi nyote pamoja? Kama ukuta unaoinama, Kama kitalu kilicho tayari kuanguka,Hufanya shauri kumwangusha tu katika cheo chake; Huufurahia uongo. Kwa kinywa chao hubariki; Kwa moyo wao hulaani. Nafsi yangu, umngoje Mungu peke yake kwa kimya. Tumaini langu hutoka kwake. Yeye tu ndiye mwamba wangu na wokovu wangu, Ngome yangu, sitatikisika sana.”

 

5.       Iamuru nasfi yako kumuhimidi Bwana na kutokusahau fadhili zake - Zaburi 103:1-5 “Ee nafsi yangu, umhimidi Bwana. Naam, vyote vilivyo ndani yangu Vilihimidi jina lake takatifu. Ee nafsi yangu, umhimidi Bwana, Wala usizisahau fadhili zake zote. Akusamehe maovu yako yote, Akuponya magonjwa yako yote, Aukomboa uhai wako na kaburi, Akutia taji ya fadhili na rehema, Aushibisha mema uzee wako, Ujana wako ukarejezwa kama tai;”

Ikumbushe nafsi yako kuwa haitakiwi kubaki chini hata kama kuna changamoto za aina gani zinakukabili, Mungu yuko kwa hiyo kama nafsi yako inaweza kuinama yuko Mungu mwenye uwezo wa kuiinua, kama nafsi yako inaweza kulia yuko Mungu anayeweza kuifanya ikaimba sifa, kama nafsi yako inaweza kukata tamaa yuko Mungu mwamba wa wokovu wako anaweza kuleta tumanini, kama nafsi yako inaweza kusumbuka na kuelemewa yuko Mungu anayeweza kuleta furaha na kuipa raha nafsi yako, Neno la Mungu linakutaka umtumainie Bwana na kumsifu hata wakati wa changamoto kali za maisha inuka acha kuketi chini tunaye Mungu aliye karibu wala hajakuacha yeye ni kimbilio na nguvu na msaada uonekanao tele wakati wa mateso hivyo hupaswi kuogopa lolote, hata nchi itetemeke, hata milima itikisike, hata moyo wa bahari uumuke yuko Mungu ambaye ukimtegemea na kumtumaini Moyo wako hauwezi kufadhaika kamwe yeye hatakuangusha  kamwe hatakuacha wala hatakupungukia, usikate tamaa, usione kuwa mazingira ni magumu, Mungu yuko kila mahali sio Yerusalem peke yake uwepo wa Mungu uko hata mapangoni, hata ukimbizini atakushika, utainuka.

“Mungu yuko hapa, Yesu Kristo  naye yuko hapa, Roho wake Mungu  yuko hapa na malaika wako hapa,x2 kwa nini mimi niteseke  na hali wewe uko hapa, usiniache uniguse mana Mungu yuko hapa, kwanini mimi nipate tabu, nidharauliwe na kutupwa hovyo usiniache uniguse, maana Mungu yuko hapa” 

Rev. Innocent Samuel Kamote

Mkuu wa wajenzi mwenye Hekima

Jumapili, 5 Julai 2026

Kwa kuwa sasa Bwana ametufanyia nafasi!


Mwanzo 26:19-22 “Watumwa wa Isaka wakachimba katika lile bonde, wakapata kisima cha maji yanayobubujika. Wachungaji wa Gerari wakagombana na wachungaji wa Isaka wakisema, Maji haya ni yetu. Ndipo akakiita jina la kile kisima Eseki, kwa sababu waligombana naye. Wakachimba kisima kingine, wakagombania na hicho tena. Akakiita jina lake Sitna. Akaondoka huko akachimba kisima kingine, wala hicho hawakukigombania. Akakiita jina lake Rehobothi, akasema, Kwa kuwa sasa BWANA ametufanyia nafasi, nasi tutazidi katika nchi.”




Utangulizi:

Ni muhimu kufahamu kuwa mtu awaye yote anapokuwa amebarikiwa na Mungu, au kama Mungu yuko pamoja na yeye anaweza kupitia vipingamizi vya aina mbalimbali katika maisha, watu wa Mungu wakati mwingine watapitia chuki zisizokuwa za kawaida, kuonewa wivu, na wakati mwingine kupitia mapambano mengi, Maisha ya Isaka ni mojawapo ya mfano wa matukio kama hayo, baada ya kuwa Mungu amemfungulia milango ya Baraka na uhuru, kutoka katika kuandamwa na vita na chuki na wivu wa maisha kutoka kwa wafilisti, Waligombania na kumpokonya visima vyake viwili yaani maji ya Eseki na Stina, hatimaye alipata maji sehemu nyingine ambapo alipaita Rehoboth akitangaza kwa imani kuwa sasa Bwana amemfanyia nafasi!, kwani kisima hicho hakikugombaniwa tena.

Mwanzo 26:19-22 “Watumwa wa Isaka wakachimba katika lile bonde, wakapata kisima cha maji yanayobubujika. Wachungaji wa Gerari wakagombana na wachungaji wa Isaka wakisema, Maji haya ni yetu. Ndipo akakiita jina la kile kisima Eseki, kwa sababu waligombana naye. Wakachimba kisima kingine, wakagombania na hicho tena. Akakiita jina lake Sitna. Akaondoka huko akachimba kisima kingine, wala hicho hawakukigombania. Akakiita jina lake Rehobothi, akasema, Kwa kuwa sasa BWANA ametufanyia nafasi, nasi tutazidi katika nchi.”

Leo tutachukua muda kujifunza na kutafakari kwa kina kuhusiana na maisha ya Isaka ambayo kimsingi yanatufundisha kuwa maisha ya watu wa Mungu na watu wa kawaida yana changamoto za aina mbalimbali lakini hata hivyo tunapoendelea kumtegemea Mungu hatimaye Mungu hutupa ahueni, tutajifunza somo hili Kwa kuwa sasa Bwana ametufanyia nafasi kwa kuzingatia vipengele muhimu vitatu vifuatayo:-

·         Maana ya maneno Bwana ametufanyia nafasi

·         Maisha ya changamoto za mtu wa Mungu

·         Kwa kuwa sasa Bwana ametufanyia nafasi


Maana ya maneno Bwana ametufanyia nafasi.

Maneno Kwa kuwa Bwana ametufanyia nafasi  kwa Kiebrania “Rehoboth” yalitamkwa na Isaka yakimaanisha majira ya Mungu ya kuwapa watu wake mpenyo, pumziko la kiroho, nafasi ya kukua, nafasi ya kuongezeka, nafasi ya kuwa na Amani, nafasi ya kutokuweko katika migogoro, nafasi ya kustawi pasipokuwa na upinzani, nafasi ya thamani na utulivu, kwa hiyo neno “Rehoboth” au “Rechovoth” la Kiebrania lina maana ya Nafasi kubwa, eneo la kukua na kupanuka, uhuru wa kutenda bila upinzani, nafasi ya kustawi, na nafasi ya kuwa nje ya vikwazo, hali hii haisababishwi na akili za kibinadamu bali inasababishwa na Mungu anapoingilia kati na kundoa shinikizo na msongamano wa changamoto ili kutoa utulivu kwa watu wake, huu ni mchakato wa kuondoka katika mashinikizo kadhaa ya maisha yanayopelekea kuifikia ndoto ya utulivu unaohitajika kibinadamu.

Mungu alimpa nafasi Rehoboth Yusufu baada ya mapito ya muda mrefu katika maisha kwa kusudi la kufikia hatima yake - Mwanzo 41:38-41 “Farao akawaambia watumwa wake, Tupate wapi mtu kama huyu, mwenye roho ya Mungu ndani yake? Farao akamwambia Yusufu, Kwa kuwa Mungu amekufahamisha hayo yote, hapana mwenye akili na hekima kama wewe. Basi wewe utakuwa juu ya nyumba yangu, na kwa neno lako watu wangu watatawaliwa. Katika kiti cha enzi tu nitakuwa mkuu kuliko wewe. Farao akamwambia Yusufu, Tazama, nimekuweka juu ya nchi yote ya Misri.”

Mungu alimpa nafasi Daudi nafasi ya kutoka katika hali duni ya kuchunga kondoo na kudharaulika katika familia mpaka kuwa mfalme katika Israel – 1Samuel 16:11-13 “Kisha Samweli akamwambia Yese, Watoto wako wote wapo hapa? Naye akasema, Amesalia mdogo wao, na tazama, anawachunga kondoo. Basi Samweli akamwambia Yese, Tuma watu, wamlete; kwa sababu hatutaketi hata atakapokuja huku. Basi akatuma mtu, naye akamleta kwao. Naye alikuwa mwekundu, mwenye macho mazuri, na umbo lake lilikuwa la kupendeza. Bwana akasema, Ondoka, umtie mafuta; maana huyu ndiye.Ndipo Samweli akaitwaa pembe yenye mafuta, akamtia mafuta kati ya ndugu zake; na roho ya Bwana ikamjilia Daudi kwa nguvu tangu siku ile. Basi Samweli akaondoka, akaenda zake Rama.”

Mungu anapokufanyia nafasi au kukuletea “Rehoboth” anakuweka katika mahali ambapo adui zako hawawezi kuzuia maendeleo na ustawi wako, Milango iliyokuwa imefungwa au iliyokuwa inakutana na upinzani huanza kufunguka na kupata upenyo, Milango ya Baraka huanza kutiririka kwa urahisi, miguu yako inawekwa mahali palipoinuka na hakuna taabu tena ya kupita katika mabonde

Zaburi 31:7-8 “Na nishangilie, nizifurahie fadhili zako, Kwa kuwa umeyaona mateso yangu. Umeijua nafsi yangu taabuni, Wala hukunitia mikononi mwa adui; Miguu yangu umeisimamisha panapo nafasi.”

Maisha ya changamoto za mtu wa Mungu

Kabla Isaka hajapata utulivu wa maisha “Rehoboth” alipitia changamoto nyingi sana ambazo wakati mwingine hata watu wengine wa Mungu wanapitia, hii inamaanisha kuwa changamoto ni sehemu ya kawaida ya maisha ya mwanadamu lakini hata hivyo tukimtegemea Mungu atajitokeza hatimaye na kutupatia nafasi

·         Isaka alipoteza mama yake mpendwa Sara -  Jambo hili liliumiza sana maisha yake kama wote tunavyofahamu unapoondokewa na wazazi, moyo unauma sana na unagubikwa na upweke mkubwa  hata hivyo ujio wa Rebeka katika maisha ya Isaka ulimpa unafuu katika changamoto hiyo

 

Mwanzo 24:67 “Isaka akamwingiza Rebeka katika hema ya mama yake, Sara, akamtwaa Rebeka, akawa mkewe, akampenda; Isaka akafarijika kwa ajili ya kufa kwa mamake.”

 

·         Isaka alipitia kipindi cha kukosa mtoto miaka 20 – Baada ya Rebeka kuwa faraja kwa muda sasa wanakutana na changamoto nyingine katika maisha na sasa wanakosa mtoto kwa muda wa miaka 20, Isaka alimuoa Rebeka akiwa na miaka 40 na alikuja kupata watoto Esau na Yakobo akiwa na miaka 60, hiki ni kipindi cha kupimwa imani na uvumilivu, na ni mpaka Isaka alipomuomba Mungu ndipo Mungu alipojibu maombi na watoto mapacha wakapatikana

 

Mwanzo 25:19-28 “Na hivi ndivyo vizazi vya Isaka, mwana wa Ibrahimu. Ibrahimu alimzaa Isaka. Isaka akawa mwenye miaka arobaini alipomtwaa Rebeka binti Bethueli, Mshami, wa Padan-aramu, ndugu wa Labani, Mshami, kuwa mke wake. Isaka akamwomba BWANA kwa ajili ya mke wake, maana alikuwa tasa. Naye BWANA akamwitikia, na Rebeka mkewe akachukua mimba. Watoto wakashindana tumboni mwake. Naye akasema, Ikiwa ni hivi, kuishi kwanifaa nini? Akaenda kumwuliza BWANA. BWANA akamwambia, Mataifa mawili yamo tumboni mwako, Na kabila mbili za watu watafarakana tangu tumboni mwako. Kabila moja litakuwa hodari kuliko la pili, Na mkubwa atamtumikia mdogo. Siku zake za kuzaa zilipotimia, tazama! Mapacha walikuwamo tumboni mwake. Wa kwanza akatoka, naye alikuwa mwekundu mwili wote kama vazi la nywele. Wakamwita jina lake Esau. Baadaye ndugu yake akatoka, na mkono wake unamshika Esau kisigino. Akaitwa jina lake Yakobo. Isaka alikuwa mwenye miaka sitini mkewe alipowazaa. Watoto wakakua, Esau alikuwa mtu ajuaye kuwinda wanyama, mtu wa nyikani, na Yakobo alikuwa mtu mtulivu, mwenye kukaa hemani. Basi Isaka akampenda Esau, kwa sababu alikula mawindo yake, na Rebeka akampenda Yakobo.”

 

·         Isaka alikabiliwa na njaa kubwa katika inchi – Akiwa katika nchi ya ahadi Isaka anakumbwa na njaa kali sana, njaa kama ya siku za baba yake Abrahamu ambayo ilimpelekea Abrahamu kukimbilia Misri hata hivyo kwa neema ya Mungu, Mungu alisema na Isaka asishuke kwenda Misri kama ilivyokuwa kwa baba yake, Mungu aliamua kumbariki pale pale  mahali ambapo wengine walikuwa hawana matumaini.

 

Mwanzo 26:1-5 “Ikawa njaa katika nchi hiyo, mbali na njaa ile ya kwanza iliyokuwa siku za Ibrahimu. Isaka akamwendea Abimeleki, mfalme wa Wafilisti, huko Gerari. BWANA akamtokea, akasema, Usishuke kwenda Misri, kaa katika nchi nitakayokuambia. Kaa ugenini katika nchi hiyo, nami nitakuwa pamoja nawe, na kukubariki, maana nitakupa wewe na uzao wako nchi hizi zote. Nami nitakifanya imara kiapo nilichomwapia Ibrahimu baba yako. Nitazidisha uzao wako kama nyota za mbinguni, nami nitawapa uzao wako nchi hizi zote, na katika uzao wako mataifa yote ya dunia watajibarikia. Kwa sababu Ibrahimu alisikia sauti yangu, akayahifadhi maagizo yangu, na amri zangu, na hukumu zangu, na sheria zangu.”

 

·         Isaka alikabiliwa na kuonewa wivu (Husuda) na wafilisti – Mungu alimbariki sana Isaka baada ya kubaki katika inchi ya Mkanaani, Mungu alikuwa amemuwezesha Isaka kuchimba visima vya baba yake Ibrahimu na kumsaidia kwa kutumia maji yanayobubujika kufanya kilimo cha umwagiliaji na kujipatia mazao na kuwanywesha mifugo hivyo kukawa na mafanikio makubwa sana hata wakati wa njaa Isaka alipanda kipimo cha mbegu na kuvuna mara mia, hivyo mtu huyu akawa mkuu mno na hapo ndipo Wafilisti wakamuonea wivu, kumbe kadiri Mungu anavyokubariki sana na kukuinua juu ndivyo Baraka zako zinavyoambatana na upinzani kutoka kwa watu wenye wivu wenye uchungu

 

Mwanzo 26:12-14 “Isaka akapanda mbegu katika nchi ile, akapata mwaka ule vipimo mia kwa kimoja, BWANA akambariki. Na mtu huyu akawa mkuu, akazidi kusitawi, hata akawa mkuu sana. Akawa na mali ya kondoo, na mali ya ng'ombe, na watumwa wengi. Hao Wafilisti wakamhusudu.”

 

·         Isaka alipambana na jaribu la kufukiwa kwa visima vyake – Bila shaka wafilisti walibaini kuwa utajiri wa Isaka na mafanikio makubwa aliyokuwa nayo ni uwepo wa Mungu na vile vile visima alivyokuwa amechimba na vikawa vinabubujisha maji, Wafilisti waliamua kuvifukia  visima  vyote ambavyo kimsingi vilikuwa vya baba yake yaani Abrahamu, Wafilisti walivifukia, wakati wote shetani atataka kufukia kila chanzo cha Baraka kwa watu wa Mungu ili usitoke

 

Mwanzo 26:15-21 “Na vile visima vyote walivyochimba watumwa wa baba yake, siku za Ibrahimu babaye, Wafilisti walikuwa wamevifukia, wakavijaza kifusi. Abimeleki akamwambia Isaka, Utoke kwetu, maana wewe una nguvu sana kuliko sisi. Basi Isaka akatoka huko akapiga kambi katika bonde la Gerari, akakaa huko.Isaka akarudi akavichimbua vile visima vya maji walivyovichimba siku za Ibrahimu babaye; maana wale Wafilisti walikuwa wamevifukia baada ya kufa kwake Ibrahimu; naye akaviita majina kufuata majina alivyoviita babaye.Watumwa wa Isaka wakachimba katika lile bonde, wakapata kisima cha maji yanayobubujika. Wachungaji wa Gerari wakagombana na wachungaji wa Isaka wakisema, Maji haya ni yetu. Ndipo akakiita jina la kile kisima Eseki, kwa sababu waligombana naye. Wakachimba kisima kingine, wakagombania na hicho tena. Akakiita jina lake Sitna.”

 

·         Isaka alifukuzwa kwa sababu ua ukuu wake -  Isaka alibarikiwa sana na kuwa mtu mkubwa sana, uwepo wa Mungu ulikuwa pamoja naye, upako na karama zilikaa juu yake, hakuwa mtu wa vita alikuwa mtu wa utulivu na mtu wa Amani lakini hata hivyo adui zake walishindwa kumstahimili na hivyo waliamua kumfukuza, ziko nyakati ambazo unaweza kukataliwa bila sababu au unaweza kutengenezewa zengwe ili usiwepo katika maeneo hayo na sababu kubwa watu wanadhani ukuu wako unatokana na hapo ulipo, lakini sio hivyo tu watu wema wakati mwingine hukataliwa na hata kuuawa kwa sababu ya wema wao

 

Mwanzo 26:13-16 “Na mtu huyu akawa mkuu, akazidi kusitawi, hata akawa mkuu sana. Akawa na mali ya kondoo, na mali ya ng'ombe, na watumwa wengi. Hao Wafilisti wakamhusudu. Na vile visima vyote walivyochimba watumwa wa baba yake, siku za Ibrahimu babaye, Wafilisti walikuwa wamevifukia, wakavijaza kifusi. Abimeleki akamwambia Isaka, Utoke kwetu, maana wewe una nguvu sana kuliko sisi.”

 

·         Isaka alinyimwa nafasi – Mgogoro wa visima pamoja na kufukuzwa katika nchi ya Wafilisti wakati wote ilikuwa inalenga kumnyima Isaka ustawi, adui alikuwa anawekwa vikwazo ili kumnyima Isaka fursa ya utulivu na mafanikio, waligombea kisima cha kwanza akakiita Eseki maana yake UGOMVI, walifukia kisima cha pili na kukigombea akakiita Sitna maana yake UADUI kwa hiyo utaona Isaka anakabiliwa na ugomvi, uadui, upinzani, chuki na husuda, lakini kwa jinsi alivyokuwa muungwana na mwororo, hakugombana na mtu, tunajifunza ya kuwa tunaweza kushinda vita vingi kwa kuwa waungwana na kwa kutumia hekima kuliko kushindana na kujiingiza kwenye migogoro, kutokana na utulivu huu hatimaye Mungu aliamua kumpa utulivu halisi na hapa ndipo Bwana alipompa Nafasi, Rehoboth

 

Mwanzo 26:17-22 “Basi Isaka akatoka huko akapiga kambi katika bonde la Gerari, akakaa huko. Isaka akarudi akavichimbua vile visima vya maji walivyovichimba siku za Ibrahimu babaye; maana wale Wafilisti walikuwa wamevifukia baada ya kufa kwake Ibrahimu; naye akaviita majina kufuata majina alivyoviita babaye. Watumwa wa Isaka wakachimba katika lile bonde, wakapata kisima cha maji yanayobubujika. Wachungaji wa Gerari wakagombana na wachungaji wa Isaka wakisema, Maji haya ni yetu. Ndipo akakiita jina la kile kisima Eseki, kwa sababu waligombana naye. Wakachimba kisima kingine, wakagombania na hicho tena. Akakiita jina lake Sitna. Akaondoka huko akachimba kisima kingine, wala hicho hawakukigombania. Akakiita jina lake Rehobothi, akasema, Kwa kuwa sasa BWANA ametufanyia nafasi, nasi tutazidi katika nchi.”            

Kwa kuwa sasa Bwana ametufanyia nafasi

Mpenzi maisha ya Isaka  yanamkumbusha kila mmoja wetu kuwa changamoto unazozipitia ni za kawaida, kila mtu wa Mungu anaweza kupitia changamoto za iana mbalimbali katika maisha, Yesu alisema ulimwenguni mnayo dhiki, kwa sababu hiyo dhiki kama hizi ni za kawaida kwa watu wa Mungu, hata hivyo tunapoendelea kuwa na subira na kumtegemea Mungu hatimaye Mungu atatufanyia nafasi REHOBOTH Isaka kwa kweli hakuzitegemea akili zake mwenyewe, tunaweza kukiri kuwa kweli alikuwa na taaluma ya kuchimba visima lakini taaluma hiyo ingeweza kuigizwa na wengine au kusambazwa lakini hii ilikuwa ni ishara ya kuwa Mungu alikuwa pamoja naye, ukiri wake na kauli yake haikuwa kuwa sasa tumetoboa na badala yake alikiri kuwa ni Mungu ndiye aliyewafanyia  nafasi. Isaka aliendelea kubarikiwa mpaka adui zake walikuja kujipendekeza na kufanya Amani naye huku wakitambua kuwa hakika alikuwa na Mungu

Mwanzo 26:22-29 “Akaondoka huko akachimba kisima kingine, wala hicho hawakukigombania. Akakiita jina lake Rehobothi, akasema, Kwa kuwa sasa BWANA ametufanyia nafasi, nasi tutazidi katika nchi. Akapanda kutoka hapo mpaka Beer-sheba. BWANA akamtokea usiku uleule, akasema, Mimi ni Mungu wa Ibrahimu baba yako, usiogope, maana mimi ni pamoja nawe, nami nitakubarikia, na kuzidisha uzao wako kwa ajili ya Ibrahimu mtumishi wangu. Akajenga madhabahu huko, akaliitia jina la BWANA. Akapiga hema yake huko, na watumwa wa Isaka wakachimba kisima huko. Ndipo Abimeleki akamwendea kutoka Gerari, pamoja na Ahuzathi rafiki yake, na Fikoli, jemadari wa jeshi lake. Isaka akawauliza, Mbona mwanijia, nanyi mmenichukia, mkanifukuza kwenu?Wakasema, Hakika tuliona ya kwamba BWANA alikuwa pamoja nawe; nasi tukasema, Na tuapiane, sisi na wewe, na kufanya mapatano nawe ya kuwa hutatutenda mabaya, iwapo sisi hatukukugusa wewe, wala hatukukutendea ila mema, tukakuacha uende zako kwa amani; nawe sasa u mbarikiwa wa BWANA.”

Mambo ya kujifunza kutokana na maisha ya Isaka hapo:-

1.       Mungu ndiye anayetengeneza nafasi – Isaka hakusema kwamba tumetoboa, au tumewapiga bao Wafilisti au hawatuwezi hapana, yeye alisema sasa Bwana ametufanyia nafasi na tutazidi kuongezeka alisema haya kutokana na amani kwamba sasa maadui waliogopa kumfuatilia, dhamiri zao ziliwashitaki kwamba wataendelea na dhuluma zao mpaka lini mafanikio ya kweli ni yale ambayo Bwana ndiye anayekupigania, adui zako wanatamani usiwepo lakini wewe unaendelea kustawi na sababu ya ustawi wako inagunduliwa wazi kuwa ni Mungu, Mungu akikuandalia mazingira inapendeza sana kuliko wewe mwenyewe ukijilazimishia mazingira ya mafanikio

 

Zaburi 127:1 “Bwana asipoijenga nyumba Waijengao wafanya kazi bure. Bwana asipoulinda mji Yeye aulindaye akesha bure.”          

 

2.       Mafanikio ya kweli yanahitaji uvumilivu – wako watu ambao wanatamaa ya mafanikio na wanadhani kuwa mafanikio yanakuja kwa kuamka tu asubuhi, au kwa kuyalazimisha, nimeona watu wengi sana hasa vijana wanataka kila kitu kitokee kwa haraka lakini ni muhimu kuwa wavumilivu na kuwa wenye subira kwa sababu Mungu sio dhalimu kwa wakati wake atafanya, Isaka alivumilia, dhihaka, utasa, huzuni, njaa, wivu, ugomvi, kufukuzwa, uadui, dhuluma na kadhalika, alikuwa na nguvu kubwa sana lakini hakuitumia kupigana na adui zake  na kisha Bwana mwenyewe alimfanyia nafasi, hatupaswi kujipigania, hatupawi kukata tamaa hata kama Eseki na Sitna zitatokea katika maisha yetu hatimaye REHOBOTH italetwa na Bwana  kila mtu wa Mungu ajifunze ya kuwa anahitaji uvumilivu Saburi na mambo hayatakuja kuwa wakati mwingine kwa haraka kama tunavyofikiri

 

3.       Mungu anapokufungulia mlango Rehoboth - anakutengenezea mazingira ya kuongezeka, anakufanya ukue, huduma yako itakua, familia yako itaongezeka, uchumi wako utakuwa, Kiroho utakuwa, ushawishi utaiongezeka  utaogopwa, utaabudu kwa Amani na usalama, utafutwa machozi, adui zako watakuja kupatana na wewe wao wenyewe, utafurahia ndoa yako, utamfurahia Bwana Mungu wako, utafurahia biashara zako, utafurahia mifugo na kilimo, utaongeza maarifa hekima na elimu, utatimiza makusudi ya Mungu utakuwa na shuhuda, utatumika  

 

Zaburi 4:1-5 “Ee Mungu wa haki yangu, uniitikie niitapo; Umenifanyizia nafasi wakati wa shida; Unifadhili na kuisikia sala yangu. Enyi wanadamu, hata lini utukufu wangu utafedheheka? Je! Mtapenda ubatili na kutafuta uongo? Bali jueni ya kuwa Bwana amejiteulia mtauwa; Bwana atasikia nimwitapo. Mwe na hofu wala msitende dhambi, Tafakarini vitandani mwenu na kutulia. Toeni dhabihu za haki, Na kumtumaini Bwana

Ndugu zangu wapenzi kaka zangu na dada zangu, haijalishi ni maisha ya namna gani unayapitia, tambua tu kuwa dunia haina huruma hata kidogo na maisha yako, ni lazima umuwekee Mungu tumaini lako, unapojikita katika kumtegemea Mungu na kujiepusha na migogoro kisha wewe kuwa sababu ya Amani Mungu wa Ibrahimu, na wa Isaka na Yakobo baba zetu hatatuacha dunia yote na kila mtu anayesikia shuhuda zako atajua wazi kuwa Bwana yuko pamoja nawe, Bwana atakupigania nawe utanyamaza kimya, adui zako watakuja kukusujudia, hiki ndicho kilichomtokea Isaka Bwana alikuwa pamoja naye mpaka adui zake walilitambua hilo na kufanya Amani naye, wewe hupigani mwenyewe yuko anayekupigania naye yu hai katika jina la Yesu Kristo mwana wa Mungu aliye hai, Amen!

Na. Rev. Innocent Samuel Kamote.

Mkuu wa wajenzi mwenye Hekima.

Jumapili, 28 Juni 2026

Mwenende kama ulivyo wajibu wenu kwa Bwana!


Wakolosai 1:9-11 “Kwa sababu hiyo sisi nasi, tangu siku ile tuliposikia, hatuachi kufanya maombi na dua kwa ajili yenu, ili mjazwe maarifa ya mapenzi yake katika hekima yote na ufahamu wa rohoni; MWENENDE KAMA ULIVYO WAJIBU WENU KWA BWANA, mkimpendeza kabisa; mkizaa matunda kwa kila kazi njema, na kuzidi katika maarifa ya Mungu; mkiwezeshwa kwa uwezo wote, kwa kadiri ya nguvu ya utukufu wake, mpate kuwa na saburi ya kila namna na uvumilivu pamoja na furaha; mkimshukuru Baba, aliyewastahilisha kupokea sehemu ya urithi wa watakatifu katika nuru.”

 



Utangulizi:

Ni muhimu kufahamu kuwa mara baada ya kuwa tumeokolewa kwa neema ya Mungu, kwa njia ya imani, tunapaswa sana kuzingatia mwenendo wetu, Mtu aliyeokoka hataishi maisha anayojitakia tu kwa sababu ameokolewa, Lakini maandiko yanatoa maelekezo ya jinsi tunavyopaswa kuishi, yaani uko wajibu wetu tunaopaswa kutembea katika huo ili tuweze kuwa mfano wa kuigwa kama wana wa Mungu tuwapo hapa ulimwenguni, mwenendo huo ni wa lazima na wala sio wa hiyari, tunapaswa kuendenda kama vile Yesu Kristo mwenyewe alivyoenenda hapa duniani.

 

1Yohana 2:4-6 “Yeye asemaye, Nimemjua, wala hazishiki amri zake, ni mwongo, wala kweli haimo ndani yake. Lakini yeye alishikaye neno lake, katika huyo upendo wa Mungu umekamilika kweli kweli. Katika hili twajua ya kuwa tumo ndani yake. Yeye asemaye ya kuwa anakaa ndani yake, imempasa KUENENDA mwenyewe vile vile kama yeye ALIVYOENENDA.”

 

Katika maandiko yetu ya Msingi Paulo mtume anawaandikia Wakolosai aina ya maombi anayowaombea na kuwalekeza watu hao wajazwe maarifa ya mapenzi yake katika hekima yote na ufahamu wa rohoni ili kwamba waenende kama ulivyo wajibu wao kwa Bwana wakimpendeza yeye Kabisa!, Kumbe tunagundua ya kuwa kuna namna basi Wakristo tunapaswa kuenenda na swala hili liko wazi kabisa katika neno la Mungu. Kuna namna ya kutembea katika ulimwengu huu

 

Wafilipi 2:14-15 “Yatendeni mambo yote pasipo manung'uniko wala mashindano, mpate kuwa wana wa Mungu wasio na lawama, wala udanganyifu, wasio na ila kati ya kizazi chenye ukaidi, kilichopotoka; ambao kati ya hao mnaonekana kuwa kama mianga katika ulimwengu,”

 

Tito 2:11-12 “Maana neema ya Mungu iwaokoayo wanadamu wote imefunuliwa; nayo yatufundisha kukataa ubaya na tamaa za kidunia; tupate kuishi kwa kiasi, na haki, na utauwa, katika ulimwengu huu wa sasa;

 

Wakolosai 2:4-6 “Nasema neno hili, mtu asije akawadanganya kwa maneno ya kuwashawishi. Maana nijapokuwa sipo kwa mwili, lakini nipo pamoja nanyi kwa roho, nikifurahi na kuuona utaratibu wenu na uthabiti wa imani yenu katika Kristo. Basi kama mlivyompokea Kristo Yesu, Bwana, ENENDENI vivyo hivyo katika yeye;”

 

Kwa msingi huo utaweza kuona kuwa maandiko matakatifu yana namna ambayo kwamba Roho Mtakatifu ametukusudia sisi kuenenda sawasawa na maelekezo yanayotolewa katika maandiko lakini ili tuweze kuendelea kuelewa vizuri hatuna budi kufahamu maswala kadhaa ikiwa ni pamoja na maana ya neno mwenendo, tutajifunza somo hili Mwenende kama ulivyo wajibu wenu kwa Bwana! Kwa kuzingatia vipengele muhimu vitatu vifuatavyo;-

 

·         Maana ya neno mwenendo.

·         Jinsi inavyotupasa kuenenda.

·         Mwenende kama ulivyo wajibu wenu kwa Bwana!

 

Maana ya neno mwenendo.

 

Neno mwenendo ambalo limejitokeza zaidi ya mara 13 katika maandiko ya Kiyunani linasomeka kama “AnastrophÄ“” ambalo katika Biblia ya kiingereza linasomeka kama “conversation”, au “Behavior” au “Conducts” Katika Biblia ya Kiswahili limetumika neno mawazo, au mtazamo, tabia au mwenendo  kwa mfano kabla ya kuokoka mtu anaweza kuwa na tabia au mwenendo  ua mawazo yanayomuongoza kuwa na tabia hiyo, kwa hiyo mwenendo ni jumla ya mtazamo wa mtu na mazingira yanayopelekea awe na tabia hiyo aliyo nayo, Paulo mtume kabla ya kuokoka alikuwa na mtazamo kuwa Ukristo sio imani ya kweli na kwa sababu hiyo aliwatesa sana Wakristo na kanisa la kwanza kwa sababu mtazamo wake ulipelekea kuwa na mwenendo au tabia aliyokuwa nayo kabla ya kukutana na Bwana Yesu.

 

Wagalatia 1:13Maana mmesikia habari za MWENENDO wangu zamani katika dini ya Kiyahudi, kwamba naliliudhi kanisa la Mungu kupita kiasi, nikaliharibu. Nami naliendelea katika dini ya Kiyahudi kuliko wengi walio hirimu zangu katika kabila yangu, nikajitahidi sana katika kuyashika mapokeo ya baba zangu. Lakini Mungu, aliyenitenga tangu tumboni mwa mama yangu, akaniita kwa neema yake,”

 

Kwa hiyo mtu aliyeokoka anapaswa kuwa na mabadiliko ya mwenendo wake wa kwanza au ule wa zamani na anapaswa kuvaa mwenendo mpya unaotembea katika hali ya uchaji wa Mungu kwa kuzingatia kweli, haki na utakatifu, kwa sababu hiyo mtu aliyemwamini Bwana anatarajiwa awe na mwenendo tofauti na ule aliokuwa akiuendea zamani, haya ni mabadiliko yanayoanzia kwemye mtazamo, fundisho na kuonekana katika tabia na mtazamo mpya unaompa Mungu utukufu baada ya kumpokea Yesu kama Bwana na mwokozi wa maisha yetu!

 

Waefeso 4:20-24 “Bali ninyi, sivyo mlivyojifunza Kristo; ikiwa mlimsikia mkafundishwa katika yeye, kama kweli ilivyo katika Yesu, mvue kwa habari ya MWENENDO wa kwanza utu wa zamani, unaoharibika kwa kuzifuata tamaa zenye kudanganya; na mfanywe wapya katika roho ya nia zenu; mkavae utu mpya, ulioumbwa kwa namna ya Mungu katika haki na utakatifu wa kweli.”

 

Jinsi inavyotupasa kuenenda.

 

Tumejifunza sasa maana ya mwenendo na tumeona jinsi maandiko yanavyotuelezea kuwa uko mwenendo ambao tuliuendea zamani kabla ya kuokolewa na sasa baada ya kuwa tumeokolewa kuna aina ya mwenendo ambao tunapaswa kuuenenda na bila kufundishwa wakati mwingine inaweza kuwa ngumu kwetu kujua ni mwenendo gani tunapaswa kuufuata? Kwa hiyo yako mambo kadhaa ambayo Biblia inatuasa kuyafuata au kuyajifunza ili yaweze kuwa dira na njia ya kuujenga mwenendo wetu na huo ndio wajibu wetu ambao umesisitizwa katika maandiko ya msingi kwamba Mwenende kama ulivyo wajibu wenu kwa Bwana ni wajibu upi huo hapa yako mambo kadhaa ya kuyaangalia

 

1.       Ni wajibu wetu kuenenda kwa utakatifu – Utakatifu ni moja ya mwenendo ambao watu waliookoka wanapaswa kuwa nao, ni muhimu kuelewa kuwa ni vigumu kumuona Mungu bila ya kuwa na mwenendo wa utakatifu, utakatifu ni nini hasa? Biblia ya Kiyunani inatumia neno “Hagio” ambalo ni sawa na neno la Kiingereza “Pure morally” au “Blameless  maana yake kuendenda kwa uadilifu, au kutembea bila lawama, wakati wote katika maisha yetu isitokee tumelaumiwa kama watu wabaya au kwa kutenda mambo yasiyo ya uadilifu

 

1Petro 1:14-16. “Kama watoto wa kutii msijifananishe na tamaa zenu za kwanza za ujinga wenu; bali kama yeye aliyewaita alivyo mtakatifu, ninyi nanyi iweni watakatifu katika MWENENDO wenu wote; kwa maana imeandikwa, Mtakuwa watakatifu kwa kuwa mimi ni mtakatifu.”

 

2.       Ni wajibu wetu kuendenda kwa imani – watu wa Mungu wanapaswa kuenenda kwa Imani, pasipo imani haiwezekani kumpendeza Mungu, kwa hiyo yote tuyatendayo tunapaswa kuyafanya kwa imani, Mungu aliwaangamiza wana wa Israel wengi jangwani kwa sababu ya kutokuamini kwao, tukiendenda kwa imani ni rahisi kumpendeza Mungu, watu wa Mungu wanapaswa kuliamini neno la Mungu na kulitii kwa imani na sio kwa kutegemea yale tuyaonayo kwa macho ya kibinadamu au mazingira yanayokuzunguka

 

2Wakorintho 5:6-8 “Basi siku zote tuna moyo mkuu; tena twajua ya kuwa, wakati tuwapo hapa katika mwili, tunakaa mbali na Bwana. (Maana TWAENENDA kwa imani, si kwa kuona.) Lakini tuna moyo mkuu; nasi tunaona ni afadhali kutokuwamo katika mwili na kukaa pamoja na Bwana.”

 

3.       Ni wajibu wetu kuenenda kwa Upendo – Kuenenda kwa upendo ni mojawapo ya agizo la watu wa Mungu, kuishi kwa upendo, kutembea kwa upendo kujawa na upendo maisha yetu ni lazima yaonyeshe upendo wa kujitoa kama vile Kristo alivyojitoa kwetu na kwa ulimwengu ili kila amuaminiye aokolewe, chuki, husuda na wivu, magombano, visasi na majungu kamwe sio mwenendo wanaopaswa kuwa nao watu ambao Kristo amewafia Msalabani kwa kujitoa kuliko kukuu hata tulipokuwa wenye dhambi

 

Waefeso 5:1-2 “Hivyo mfuateni Mungu, kama watoto wanaopendwa; MKAENENDE katika upendo, kama Kristo naye alivyowapenda ninyi tena akajitoa kwa ajili yetu, sadaka na dhabihu kwa Mungu, kuwa harufu ya manukato.”

 

4.       Ni wajibu wetu kuenenda nuruni – Kuenenda nuruni kwa ufupi maana yake ni kutembea kwa kuweka kipaumbele maswala na maagizo ya Mungu, Mungu ni Nuru, Yesu Kristo mwenyewe pia alisema yeye ni Nuru ya ulimwengu, kwa sababu hiyo tunapoweka kipaumbele maswala Yote ambayo Yesu Kristo ametufundisha na kumfuata, maana yake tunaendenda Nuruni, kwenda kinyume na maagizo ya neno la Mungu ni kuenenda gizani

 

1Yohana 1:5-7 “Na hii ndiyo habari tuliyoisikia kwake, na kuihubiri kwenu, ya kwamba Mungu ni nuru, wala giza lo lote hamna ndani yake.Tukisema ya kwamba twashirikiana naye, tena tukienenda gizani, twasema uongo, wala hatuifanyi iliyo kweli; bali TUKIENENDA NURUNI, kama yeye alivyo katika nuru, twashirikiana sisi kwa sisi, na damu yake Yesu, Mwana wake, yatusafisha dhambi yote.”

 

5.       Ni wajibu wetu kuenenda katika upya wa maisha – kutembea katika upya wa maisha kunamaanisha ni lazima maisha yetu yabadilike tuwe na mwenendo mpya na sio ule wa zamani, kabala ya kuokolewa, hatupaswi tena kuitumikia dhambi ambayo tuliiendea zamani kabla ya kukutana na Yesu, sasa kwa kuwa tumekutana na Yesu hatuna budi kuenenda katika upya huu wa maisha na kutembea na Mungu, uongo, ulevi, tamaa mbaya, uchafu, kiburi, masengenyo, ubinafsi na kujihesabia haki pamoja na maovu ya kila namna hayapaswi kuonekana tena kwa mtu anayewajibika kuenenda katika upya wa maisha

 

Warumi 6:4-6 “Basi tulizikwa pamoja naye kwa njia ya ubatizo katika mauti yake, kusudi kama Kristo alivyofufuka katika wafu kwa njia ya utukufu wa Baba, vivyo hivyo na sisi TUENENDE KATIKA UPYA WA UZIMA. Kwa maana kama mlivyounganika naye katika mfano wa mauti yake, kadhalika mtaunganika kwa mfano wa kufufuka kwake; mkijua neno hili, ya kuwa utu wetu wa kale ulisulibishwa pamoja naye, ili mwili wa dhambi ubatilike, tusitumikie dhambi tena;”

 

6.       Ni wajibu wetu kuenenda kwa Roho – kuenenda kwa Roho maana yake ni nini? Ni maisha ambayo Roho Mtakatifu ndiye anayetawala, kila mtu aliyeokolewa ni muhimu na lazima atoe nafasi na kumruhusu Roho Mtakatifu kuyaongoza na kuyatawala maisha yake katika kila nyanja ya maisha na kumruhusu yeye kutusaidia kukomaa kiroho na kuzaa matunda ya Roho Mtakatifu katika maisha yetu, maisha yako unayaongoza wewe mwenyewe au unamuachia Roho akuongoze? Kuenenda kwa roho ni kumuachia yeye atuongoze maisha yetu.

 

Wagalatia 5:16-23 “Basi nasema, ENENDENI kwa Roho, wala hamtazitimiza kamwe tamaa za mwili. Kwa sababu mwili hutamani ukishindana na Roho, na Roho kushindana na mwili; kwa maana hizi zimepingana, hata hamwezi kufanya mnayotaka. Lakini mkiongozwa na Roho, hampo chini ya sheria. Basi matendo ya mwili ni dhahiri, ndiyo haya, uasherati, uchafu, ufisadi, ibada ya sanamu, uchawi, uadui, ugomvi, wivu, hasira, fitina, faraka, uzushi, husuda, ulevi, ulafi, na mambo yanayofanana na hayo, katika hayo nawaambia mapema, kama nilivyokwisha kuwaambia, ya kwamba watu watendao mambo ya jinsi hiyo hawataurithi ufalme wa Mungu. Lakini tunda la Roho ni upendo, furaha, amani, uvumilivu, utu wema, fadhili, uaminifu, upole, kiasi; juu ya mambo kama hayo hakuna sheria.”

 

7.       Ni wajibu wetu kuenenda kama unavyostahili wito wetu – Kila mtu aliyeokolewa kuna namna Mungu amemuita amtumikie katika mazingira mbalimbali na huo ndio wito wako, hapa wito haimaanishi ule wito wa kumtumikia Mungu pekee, wito maalumu, unaweza kuwa Mwalimu, Polisi, Daktrari, Mtoza ushuru, Mwanasiasa na kadhalika Mungu anataka uwe na mwenendo mwema katika kila aina ya wito ulioitiwa au kokote kule unakokuweko hata kama wewe ni fundi cherehani, iko miiko ya utumishi katika kile eneo la wito wa maisha basi huko enenda kama unavyoustahili wito wako, zaidi sana katika nyumba ya Mungu  huku tukitunza amani.

 

Waefeso 4:1-3 Kwa hiyo nawasihi, mimi niliye mfungwa katika Bwana, MWENENDE kama inavyoustahili wito wenu mlioitiwa; kwa unyenyekevu wote na upole, kwa uvumilivu, mkichukuliana katika upendo; na kujitahidi kuuhifadhi umoja wa Roho katika kifungo cha amani.”

 

8.       Ni wajibu wetu kuenenda kwa Hekima – Ni kama maandiko yanatuambaia wazi kuwa muda wetu duniani sio wa kwetu ni muda wa Mungu, Ni muda ambao tumepewa kwa kusudi la kumtumikia Mungu na kutimiza kusudi lake au mapenzi yake kwa hiyo Muda ni wa maana sana kwa watu waliookoka na haupaswi kupotezwa bure, watu wanaopoteza muda wanaitwa wasio na hekima au wajinga, ni lazima tujiangalie tunautumiaje Muda hasa sisi waafrika, tunaweza kutumia muda mwingi sana kupiga soga ua kusengenya muda ambao tungeweza kuutumia kwaajili ya Mungu, kwa kuyajua mapenzi yake na kuyafanya

 

Waefeso 5:15-17 “Basi angalieni sana jinsi MNAVYOENENDA; si kama watu wasio na hekima bali kama watu wenye hekima; mkiukomboa wakati kwa maana zamani hizi ni za uovu. Kwa sababu hiyo msiwe wajinga, bali mfahamu ni nini yaliyo mapenzi ya Bwana.”

 

9.       Ni wajibu wetu kuenenda vilevile kama tulivyompokea Kristo – Kuenenda vile vile kama tulivyompokea Kristo hakumaanishi ubaki vilevile baada ya kuokoka, lakini maana yake kila siku tunapaswa kuishi vile vile sawasawa na mafundisho tunayoyapokea kwa Bwana wetu Yesu Kristo kupitia Mwalimu wa Kweli Roho Mtakatifu, huku ni kuendelea kudumisha uhusiano wetu na Mungu kwa kutii na kujileta katika neema yake kukua katika upendo, unyenyekevu na hekima na kuhakikisha kuwa haturudi nyuma tangu tulipoanza uhusiano wetu na yeye.

 

Wakolosai 2:6-7 “Basi kama mlivyompokea Kristo Yesu, Bwana, ENENDENI vivyo hivyo katika yeye; wenye shina na wenye kujengwa katika yeye; mmefanywa imara kwa imani, kama mlivyofundishwa; mkizidi kutoa shukrani.

 

10.   Ni wajibu wetu kuenenda kwa kuikulia neema – Tumeokolewa kwa neema sisi kama wana wa Mungu ni wana wa neema kwa msingi huo hatuna budi kukua kwa kuikulia neema ya Mungu ni neema ya Mungu ndiyo inayotusaidia katika, kuukulia wokovu na kukomaa kiroho kwa hiyo hatuna budi kujitoa sisi wenyewe na kuenenda kwa kuikulia neema kwa kuendelea kutenda mema

 

Waefeso 2:8-10 “Kwa maana mmeokolewa kwa neema, kwa njia ya imani; ambayo hiyo haikutokana na nafsi zenu, ni kipawa cha Mungu; wala si kwa matendo, mtu awaye yote asije akajisifu. Maana tu kazi yake, tuliumbwa katika Kristo Yesu, tutende matendo mema, ambayo tokea awali Mungu aliyatengeneza ili TUENENDE NAYO.”

 

Mwenende kama ulivyo wajibu wenu kwa Bwana!

 

Wokovu ni Msaada wa Mungu kwetu, hata hivyo tabia na mwenendo ni wajibu wetu na ndio maana neno la Mungu linasema mwenende kama ulivyo wajibu wenu kwa Bwana, ni wajibu wetu kujitoa kwa Mungu na kukubali neema ya Mungu ituendeshe katika maisha haya kama watoto wake uili tuweze kuwa na mvuto hapa ulimwenguni, mwenendo wetu una nafasi kubwa mbili, kuimarisha uhusiano wetu wa ndani na Mungu, na pili kuwavutia wengine au kuwafundisha kivitendo jinsi Mungu alivyo mwadilifu, kuenenda kama ulivyo wajibu wetu kwa Bwana kumpa Mungu heshima inayoonyesha kuwa Mungu anabadilisha  maisha ya watu wake, tunaweza kuitangaza injili hata bila kusema neno kupitia tu mwenendo mwema, aina binadamu wote duniani wanajua kiwango cha uadilifu ambao watu wa Mungu wanapaswa kuenenda na ndio maana ukifanya mambo ya ajabu wanajua, kutokana na umuhimu wa jambo hili Paulo mtume aliwaombea sana wakolosai wajazwe maarifa, na hekima na ufahamu wa rohoni ili waenende kama ulivyo wajibu wao kwa Bwana wakimpendeza kabisa sio hivyo tu wakiwavutia watu wengine wasioamini waweze kuokolewa ili hayo yatimie hatuna budi kujitoa na kuhakikisha vile vile tunajileta wenyewe kanisani katika ibada za mafundisho ili tukutane na neno la Mungu litakalotupoa hekima na maarifa ili tujue nemna inavyotupasa kuenenda

 

Wakolosai 1:9-11 “Kwa sababu hiyo sisi nasi, tangu siku ile tuliposikia, hatuachi kufanya maombi na dua kwa ajili yenu, ili mjazwe maarifa ya mapenzi yake katika hekima yote na ufahamu wa rohoni; MWENENDE KAMA ULIVYO WAJIBU WENU KWA BWANA, mkimpendeza kabisa; mkizaa matunda kwa kila kazi njema, na kuzidi katika maarifa ya Mungu; mkiwezeshwa kwa uwezo wote, kwa kadiri ya nguvu ya utukufu wake, mpate kuwa na saburi ya kila namna na uvumilivu pamoja na furaha; mkimshukuru Baba, aliyewastahilisha kupokea sehemu ya urithi wa watakatifu katika nuru.”

 

1Petro 3:1-2 “Kadhalika ninyi wake, watiini waume zenu; kusudi, ikiwa wako wasioliamini Neno, wavutwe kwa MWENENDO wa wake zao, pasipo lile Neno; wakiutazama MWENENDO wenu safi, na wa hofu.”

 

Mwenendo ni msingi muhimu sana katika maisha ya Ukristo, ni lazima kila Mkristo awe na mwenendo unaomuakisi Yesu Kristo na hii ni kanuni Muhimu sana katika maisha ya ukristo na mwenendo wa kibiblia, mwenendo mwema mbele ya watu wasiomjua Mungu huwavutia watu wengine wapate kuokolewa, na sio hivyo tu ni mwenendo ndio unaotusaidia kupata viongozi wa kanisa ambao mfano wao unaweza kuigizwa na wengine mwenendo unatajwa kama hekima na tabia nzuri, unatajwa kama utetezi tunaposingiziwa, unaonyesha kielelelzo kama viongozi katika nyumba ya Mungu kwa hivyo tukiwajibika vizuri kwa Bwana tutawavutia watu kukubali ukweli ya kuwa Mungu anaokoa na anabadilisha watu wake kwa sababu watu wataona mabadiliko makubwa ya mwenendo wetu.

 

Yakobo 3:11-13. “Je! Chemchemi katika jicho moja hutoa maji matamu na maji machungu? Ndugu zangu, Je! Mtini waweza kuzaa zeituni, au mzabibu kuzaa tini? Kadhalika chemchemi haiwezi kutoa maji ya chumvi na maji matamu. N'nani aliye na hekima na ufahamu kwenu? Na aonyeshe kazi zake kwa MWENENDO wake mzuri, katika upole wa hekima.”

 

1Timotheo 4:12 “Mtu awaye yote asiudharau ujana wako, bali uwe kielelezo kwao waaminio, katika usemi na MWENENDO, na katika upendo na imani na usafi.”

 

1Petro 2:12 “Mwe na MWENENDO mzuri kati ya Mataifa, ili, iwapo huwasingizia kuwa watenda mabaya, wayatazamapo matendo yenu mazuri, wamtukuze Mungu siku ya kujiliwa.”

 

Na Rev. Innocent Samuel Kamote

 

Mkuu wa wajenzi mwenye Hekima