Jumapili, 22 Februari 2026

Kombeo la Daudi!


1Samuel 17:38-40. “Ndipo Sauli akamvika Daudi mavazi yake ya vita, akamtia chapeo cha shaba kichwani, akamvika dirii. Naye Daudi akajifunga upanga juu ya mavazi yake, akajaribu kwenda; maana alikuwa hajavijaribu. Daudi akamwambia Sauli, Siwezi kwenda na vitu hivi, maana sikuvijaribu. Basi Daudi akavivua. Akaichukua fimbo yake mkononi, akajichagulia mawe laini matano katika kijito cha maji, akayatia katika mfuko wa kichungaji aliokuwa nao, maana ni mkoba wake, na kombeo lake alikuwa nalo mkononi mwake, akamkaribia yule Mfilisti.”




Utangulizi:

Ni muhimu kufahamu kuwa katika maisha yetu duniani wakati mwingine adui zetu watatulazimisha kuingia katika vita hata kama sisi ni watu wa Amani, na ni muhimu kwetu kujua kuwa sisi ni askari wa Yesu Kristo kwa hiyo tuwapo duniani tunapigana, tunapigana vita vita inayoonekana na isiyoonekana na kwa sababu hiyo ni lazima kila mmoja wetu apigane vita vilivyo vizuri na kuilinda Imani, Paulo mtume alipokuwa anahitimisha kazi yake ya injili duniani alitoa taarifa kuwa amevipiga vita vizuri.

2Timotheo 4:7-8 “Nimevipiga vita vilivyo vizuri, mwendo nimeumaliza, Imani nimeilinda; baada ya hayo nimewekewa taji ya haki, ambayo Bwana, mhukumu mwenye haki, atanipa siku ile; wala si mimi tu, bali na watu wote pia waliopenda kufunuliwa kwake.”

Katika vita zetu duniani ni lazima tuelewe kuwa Mungu ndiye anayetufundisha vita na kwa sababu hiyo ni muhimu kwetu kuwa makini na kujifunza kutoka kwake namna na jinsi tunavyoweza kupigana vita hizo ili tuweze kushinda.

2Samuel 22:33-35 “Mungu ndiye ngome yangu yenye nguvu; Naye huwaongoza wakamilifu katika njia yake. Huifanya miguu yangu kuwa kama ya kulungu; Na kunisimamisha mahali pangu pa juu. Ananifundisha mikono yangu vita; Hata mikono yangu yaupinda upinde wa shaba.”

Zaburi 18:31-34 “Maana ni nani aliye Mungu ila Bwana? Ni nani aliye mwamba ila Mungu wetu? Mungu ndiye anifungaye mshipi wa nguvu, Naye anaifanya kamilifu njia yangu. Miguu yangu anaifanya kuwa ya kulungu, Na kunisimamisha mahali pangu pa juu. Ananifundisha mikono yangu vita, Mikono yangu ikaupinda upinde wa shaba.”

Zaburi 144:1-2 “Na ahimidiwe Bwana, mwamba wangu, Anifundishaye mikono yangu vita, Vidole vyangu kupigana. Mhisani wangu na boma langu, Ngome yangu na mwokozi wangu, Ngao yangu niliyemkimbilia, Huwatiisha watu wangu chini yangu.”    

Mungu huwafundisha watu wake vita na namna ya kupigana kwa jina la Bwana na kupata ushindi katika maisha yetu, Moja ya watu waliokuwa na uhodari katika vita ni pamoja na Daudi na watakatifu waliotutangulia wao walikuwa hodari katika vita kwa sababu Mungu aliwafundisha namna ya kupigana kwa usahihi katika maisha haya ya mapigano dhidi ya adui yetu mkuu ambaye ni shetani, maandiko yanawataja kuwa walikuwa hodari katika vita, sisi nasi Mungu na atupe kuwa hodari katika vita sawasawa na mapenzi yake katika jina la Yesu Kristo Mwana wa Mungu aliye hai

Waebrania 11:32-33 “Nami niseme nini tena? Maana wakati usingenitosha kuleta habari za Gideoni na Baraka na Samsoni na Yeftha na Daudi na Samweli na za manabii; ambao kwa imani walishinda milki za wafalme, walitenda haki, walipata ahadi, walifunga vinywa vya simba, walizima nguvu za moto, waliokoka na makali ya upanga. Walitiwa nguvu baada ya kuwa dhaifu, walikuwa hodari katika vita, walikimbiza majeshi ya wageni.”

Leo tutachukua muda kujifunza kutoka kwa Daudi jinsi Mungu alivyoweza kumtumia kuleta ushindi mkubwa kwa watu wa Taifa lake dhidi ya wafilisti kwa kutumia silaha duni na dhaifu maarufu kama kombeo, na tutajifunza somo hili Kombeo la Daudi kwa kuzingatia vipengele vitatu vifuatavyo;-

·         Ufahamu kuhusu Kombeo

·         Kombeo la Daudi

·         Kanisa na kombeo la Daudi.


Ufahamu kuhusu Kombeo.

Mojawapo ya silaha ya zamani sana ambayo ilitengenezwa kwa kamba zilizofumwa vizuri au ngozi na kuwekewa kifuko cha ngozi katikati kwaajili ya kuwekea jiwe kisha kuzungushwa na kuliachia jiwe kwa kasi kubwa na kwa ufundi wa kulenga shabaha ni pamoja na kombeo, Kombeo kama silaha iliyotumiwa na Daudi kuleta ushindi dhidi ya Goliath sasa ina umri wa miaka kama 3000, silaha hiyo maarufu kwa lugha ya kiebania kama “Kela David”  au “Qela David” na kwa kiingereza “David Sling” Kiswahili inaweza kuitwa “Kombeo la Daudi” au “Manati ya Daudi”, ni silaha duni na ya zamani sana iliyotumiwa na watu masikini wasiokuwa na uwezo hata wa kununua panga au mkuki, ndiyo silaha iliyotumiwa na Daudi kumuua Goliathi kwa jina la Bwana wa majeshi Mungu wa Israel, jina lingine la kombeo ni teo.

1Samuel 17:43-45 “Mfilisti akamwambia Daudi, Je! Mimi ni mbwa hata umenijia kwa fimbo? Mfilisti akamlaani Daudi kwa miungu yake.Mfilisti akamwambia Daudi, Njoo huku kwangu; nyama yako nitawapa ndege wa angani na wanyama wa mwituni. Ndipo Daudi akamwambia yule Mfilisti, Wewe unanijia mimi na upanga, na fumo, na mkuki, bali mimi ninakujia wewe kwa jina la Bwana wa majeshi, Mungu wa majeshi ya Israeli uliowatukana.”

Ni ukweli uliowazi kuwa  ushindi wa Daudi dhidi ya Goliath haukusababishwa na kombeo pekee bali Mungu alihusika nyuma ya ufundi, Imani na ujasiri wa Daudi, Daudi mwenyewe alikuwa na uelewa kamili kuwa Bwana angemtia Goliath katika mikono yake akiwa na uhakika kuwa Mungu haokoi kwa upanga wala mkuki bali kwa nguvu zake.

1Samuel 17:45-47 “Ndipo Daudi akamwambia yule Mfilisti, Wewe unanijia mimi na upanga, na fumo, na mkuki, bali mimi ninakujia wewe kwa jina la Bwana wa majeshi, Mungu wa majeshi ya Israeli uliowatukana. Siku hii ya leo Bwana atakuua mkononi mwangu, nami nitakupiga, na kukuondolea kichwa chako, nami leo nitawapa ndege wa angani na wanyama wa nchi mizoga ya majeshi ya Wafilisti, ili kwamba dunia nzima wajue ya kuwa yuko Mungu katika Israeli. Nao jamii ya watu wote pia wajue ya kwamba Bwana haokoi kwa upanga wala kwa mkuki; maana vita ni vya Bwana, naye atawatia ninyi mikononi mwetu.”

Maneno  haya ya Daudi yanathibitisha kuwa kulikuwa na zaidi ya kombeo katika vita ile, watu wakati mwingine tunaweza kusema kuwa kombeo la Daudi pia linaweza kuitwa “kombeo la Bwana”, Mungu alihusika kwa asilimia zote kusababisha muujiza ule kupitia silaha duni na ya chini na ya kimasikini sana, Wakristo wakati mwingine tumepambana na maswala magumu sana duniani, na wakati mwingine na watu wakubwa sana  wenye nguvu, wenye akili, wenye utajiri na uwezo, wasemaji wazuri kuliko sisi lakini tunaweza kuwaangusha chini kwa silaha zetu duni na zenye kudharaulika endapo tutazitumia silaha hizo vema, ingawa silaha  za vita vyetu si za mwili lakini tunaelezwa katika maandiko kuwa zina uwezo katika Mungu hata kuangusha ngome na kila kitu kinachijiinu kinyume na Mungu.

2Wakorintho 10:4-6 “(maana silaha za vita vyetu si za mwili, bali zina uwezo katika Mungu hata kuangusha ngome ;) tukiangusha mawazo na kila kitu kilichoinuka, kijiinuacho juu ya elimu ya Mungu; na tukiteka nyara kila fikira ipate kumtii Kristo; tena tukiwa tayari kupatiliza maasi yote, kutii kwenu kutakapotimia.”

Pamoja na uduni wa kombeo moja ya sifa kubwa ya kombeo ilikuwa ni ni silaha ambayo kamwe haiko kwenye kundi la silaha ya kubahatisha na wale waliojifunza kuitumia wanakiri kuwa inapiga kwa ustadi na kwa umakini mkubwa, kwa hiyo Daudi alikuwa na uzoefu wa siri wa matumizi ya silaha hiyo ambayo aliitumia pia kuua dubu na simba kabla ya kujitokeza hadharani, wapendwa silaha za rohoni kama ukizitumia kwa ustadi zinalenga pale pale na kumaliza kabisa nguvu za adui bila kubahatisha, Kufunga na kuomba na matumizi sahihi ya neno la Mungu hakujawai hata siku moja kuwa kitu cha kubahatisha kama unataka kumpiga adui kwa usahihi basi tumia silaha hizo kwa usahihi.

Wajibu wa kutokuogopa silaha nzito:

Neno la Mungu limeonya kuwa hatupaswi kuogopa silaha za upande wa adui hata kama zitaonekana kuwa na ubora na manufaa kuliko silaha zetu, hatupaswi kuogopa farasi, wala magari ya vita, wala jeshi kubwa, Mungu amesema katika neno lake havipaswi kuogopewa, tunapoingia katika uwanja wa vita vya kiroho kamwe tusiogope nguvu za kibinadamu, wala teknolojia ya vita, wala ufundi wa maneno, wala takwimu ya jeshi kubwa wala uzoefu na ujuzi wa maadui, Mungu alitaka watu wake wamtegemee yeye tu yeye mwenyewe ndiye vita yetu, Mungu haokoi kwa wingi,

Kumbukumbu 20:1-4 “Utokapo kwenda vitani kupigana na adui zako, na kuona farasi, na magari, na watu wengi kuliko wewe, usiwaogope; kwa kuwa Bwana Mungu wako, yu pamoja nawe, aliyekukweza kutoka nchi ya Misri. Na iwe, msongeapo mapiganoni, kuhani na akaribie na kusema na watu, awaambie, Sikizeni, enyi Israeli, hivi leo mwasongea mapiganoni juu ya adui zenu mioyo yenu na isizime; msiche, wala msiteteme, wala msiingiwe na hofu kwa ajili ya wao; kwa maana Bwana, Mungu wenu, ndiye awaandamaye kwenda kuwapigania juu ya adui zenu, ili kuwaokoa ninyi.”

Kumbukumbu 17:16 “Ila asifanye farasi wake kuwa wengi, wala asiwarudishe watu Misri, ili apate kufanya farasi kuwa wengi; kwa kuwa Bwana amewaambia, Tangu sasa msirudie tena njia ile.”

Yoshua 11:1-11 “Kisha ikawa, hapo huyo Yabini, mfalme wa Hazori, aliposikia habari ya mambo hayo, akatuma mjumbe aende kwa Yobabu, mfalme wa Madoni, na kwa mfalme wa Shimroni, na mfalme wa Akshafu, na hao wafalme waliokuwa upande wa kaskazini, katika nchi ya vilima, na katika Araba upande wa kusini wa Kinerethi, na katika Shefela, na katika nchi zilizoinuka za Dori upande wa magharibi, na kwa Mkanaani upande wa mashariki, na upande wa magharibi, na kwa Mwamori, na Mhiti, na Mperizi na Myebusi katika nchi ya vilima, na kwa Mhivi pale chini ya Hermoni katika nchi ya Mispa. Nao wakatoka nje, wao na jeshi zao zote pamoja nao, watu wengi mno, kama mchanga ulio ufuoni mwa bahari kwa wingi, pamoja na farasi na magari mengi sana. Wafalme hao wote wakakutana pamoja; wakaenda na kupanga mahema yao pamoja hapo penye maji ya Meromu, ili kupigana na Israeli. Bwana akamwambia Yoshua, Usiche wewe kwa ajili ya hao; kwani kesho wakati kama huu nitawatoa hali wameuawa wote mbele ya Israeli; utawatema farasi zao, na magari yao utayapiga moto. Basi Yoshua akaenda, na watu wote wa vita pamoja naye, ili kupigana nao hapo penye maji ya Meromu ghafula; wakawaangukia. Bwana akawatia mkononi mwa Israeli, nao wakawapiga, na kuwafukuza hata kufikilia Sidoni ulio mkuu, na hata kufikilia Misrefoth-maimu, tena hata kufikilia bonde la Mispa upande wa mashariki; wakawapiga hata wasiwasaze hata mtu mmoja aliyesalia. Yoshua akawafanyia vilevile kama Bwana alivyomwamuru; akawatema farasi zao, na magari yao akayapiga moto.”

Wakati wote Mungu alifanya vita na adui za watu wake katika namna ya kushangaza sana, na Mungu aliwaonya watu wake kutokuzitumainia silaha za kimataifa na za kifalme, aliwataka watu wake kumtegemea yeye, aliwataka watu wake wawe na ujuzi kuwa sio wingi wa farasi unaookoa, wala sio wingi wa watu unaookoa wala sio ukubwa wa jeshi, tena aliwataka hata wasiombe msaada wa kivita kwa majirani hasa Misri  na hata wakiteka mateka aliwambia farasi zao wazikate mishipa na magari yao ya vita wayachome moto, Mungu anajua kuwa ziko silaha zizisooenakana kwa macho na hata zile zinazoonekana kwa macho na zikadharauliwa na kuonekana kuwa ni silaha duni, Ni ukweli ulio wazi, kuwa Mungu anazitumia nyuma ya mambo kufanya mambo makubwa ya kutisha na kushangaza, Mungu hakutaka watu wajisifie wingi na uwezo wao alitaka watu waelewe na wajue ya kuwa ushindi unatoka kwa Mungu.

Waamuzi 7:1-2 “Kisha Yerubaali, yaani Gideoni, na watu wote waliokuwa pamoja naye wakaondoka na mapema, wakapiga kambi yao karibu na kijito cha Harodi; na kambi ya Midiani ilikuwa upande wao wa kaskazini, karibu na mlima wa More, bondeni. Bwana akamwambia Gideoni, Watu hawa walio pamoja nawe ni wengi mno hata nikawatie Wamidiani katika mikono yao, wasije Israeli wakajivuna juu yangu wakisema, Mkono wangu mwenyewe ndio ulioniokoa.”

Mungu aliwapunguza wanajeshi waliotoka na Gideoni kutoka 32,000 hadi kufikia mia tatu 300 na alimkataza Gideoni kusudi Israel wasijivunie kuwa ushindi walioupata umetokama na wingi wao, katika vita za Bwana wingi haumtishi, wala hauhusiki na wokovu wake, Mungu aweza kutumia silaha duni na watu wachache kusababisha ushindi kwa utukufu wake na kwaajili ya jina lake ili sifa na utukufu zielekezwe kwake!

Zaburi 33:16-17 “Hapana mfalme aokokaye kwa wingi wa uwezo, Wala shujaa haokoki kwa wingi wa nguvu. Farasi hafai kitu kwa wokovu, Wala hamponyi mtu kwa wingi wa nguvu zake.”

Zaburi 20:6-7 “Sasa najua kuwa Bwana amwokoa masihi wake; Atamjibu kutoka mbingu zake takatifu.Hawa wanataja magari na hawa farasi, Bali sisi tutalitaja jina la Bwana, Mungu wetu.” 

Isaya 31:1-3 “Ole wao watelemkao kwenda Misri wapate msaada, na kutegemea farasi; watumainio magari kwa kuwa ni mengi, na wapanda farasi kwa kuwa ni hodari sana; lakini hawamwangalii Mtakatifu wa Israeli, wala hawamtafuti Bwana! Lakini yeye naye ana akili, naye ataleta uovu, wala hatayatangua maneno yake; Bali ataondoka juu ya nyumba yao watendao mabaya, na juu ya msaada wa hao watendao maovu. Basi Wamisri ni wanadamu wala si Mungu, na farasi zao ni nyama wala si roho; na Bwana atakaponyosha mkono wake, yeye asaidiaye atajikwaa, na yeye asaidiwaye ataanguka, nao wote pamoja watakoma.”

Isaya 54:15-17 “Tazama, yamkini watakusanyana; lakini si kwa shauri langu. Watu wo wote watakaokusanyana juu yako wataanguka kwa ajili yako.Tazama, nimemwumba mhunzi avukutaye moto wa makaa, akatoa silaha kwa kazi yake; nami nimemwumba mharibu ili aharibu. Kila silaha itakayofanyika juu yako haitafanikiwa na kila ulimi utakaoinuka juu yako katika hukumu utauhukumu kuwa mkosa. Huu ndio urithi wa watumishi wa Bwana, na haki yao inayotoka kwangu mimi, asema Bwana.”                 

Kombeo la Daudi

Daudi alikuwa na ujuzi fulani kuhusu Mungu na maagizo yake katika Torati. Alikuwa amekwisha kujifunza kuwa Mungu haokoi kwa upanga wala mkuki, alikuwa na ujuzi kuwa Mungu haokoi kwa kutumia wingi, kwa hiyo alipomwendea adui yake alikuwa na mkoba wa ngozi na ndani yake alikuwa amekunja kombeo yake na alikuwa na mawe matano laini kutoka mtoni, yanaitwa mawe laini kwa sababu yalikuwa na uduara flani yaani yasiyoweza kukata au kuumiza kutokana na kudongoroshwa katika maji, lakini yalikuwa magumu sana, Wakati Goliath alikuwa na vifaa vya kisasa  vya vita, na katika Israel ni mfalme Sauli tu na mwanae Jonathan ndio waliokuwa na uwezo wa kumiliki upanga, watu wengine wote walikuwa na silaha duni na za kimasikini, Daudi alikuwa anatambua kuwa vita ni ya Bwana na kuwa Bwana angewaliwapigania watu wake kwa hiyo Kombeo la Daudi ilikuwa ni silaha inayoonekana ya Mungu asiyeonekana, kulikuwa na kitu cha ziada katika kombeo la Daudi, yeye alionekana ameshika fimbo tu mpaka pale alipoichomoa kombeo lake na kuchagua jiwe laini na adui alisambaratishwa kwa uwezo wa jina la Bwana kupitia jiwe lile moja tu kati ya mawe matano aliyokuwa ameyachagua, kwanini Daudi alikuwa na uhakika wa silaha ile duni kumpa ushindi mkubwa usiokuwa wa kawaida?

-          Daudi alikuwa amefundishwa kupigana, Mungu alimfundisha Daudi vita na matumizi ya silaha zile duni na zikaonyesha uwezo mkubwa akiwa nyikani, wakati akiwa anachunga kondoo wa baba yake alikuwa amekwisha kujifunza kutumia kombeo, na aliona kombeo ikiwashughulikia Dubu na Simba wanyama ambao ni wakali, aliweza kupambana nao na Mungu akimsaidia, Mungu alimuokoa na wanyama hao wakali

 

1Samuel 17:34-37 “Daudi akamwambia Sauli, Mtumishi wako alikuwa akichunga kondoo za baba yake, na alipokuwa akija simba, au dubu, akamkamata mwana-kondoo wa lile kundi, mimi hutoka nikamfuata, nikampiga, nikampokonya kinywani mwake; na akinirukia, humshika ndevu zake, nikampiga, nikamwua. Mtumishi wako alimwua simba na dubu pia; na huyu Mfilisti asiyetahiriwa atakuwa kama mmoja wao, kwa sababu amewatukana majeshi ya Mungu aliye hai. Daudi akasema, Bwana aliyeniokoa na makucha ya simba, na makucha ya dubu, ataniokoa na mkono wa Mfilisti huyu. Sauli akamwambia Daudi, Enenda, na Bwana atakuwa pamoja nawe.”

 

-          Daudi hakutegemea silaha za kifalme, Kulikuwa na nyakati ambapo wafilisti walihodhi teknolojia ya usindikaji vyuma kwa kusudi la kuwazuia Waisrael wasitengeneze silaha, hii ilikuwa mbinu ya kimkakati ya adui ya kuwafanya Israel wawe dhaifu na tegemezi, kwa hiyo watu walioweza kumiliki silaha za vyuma walikuwa ni wafalme au watu matajiri sana wenye kipato cha hali ya juu, kwa hiyo mtu kama Daudi hakuwa na uwezo wa kumiliki silaha za chuma wala hakuwa na ujuzi katika hizo, ilikuwa mtu akitaka kunoa hata jembe ni lazima aende kwa wafilisti, kwa hiyo uhodari wa vita ulikuwa ni katika matumizi ya kombeo, fimbo mawe na vifaa vya shambani, wafilisti walitaka kuwanyima Israel maarifa na dhana za mapigano  ili kujihakikishia ushindi

 

1Samuel 13:19-22 “Basi, hakuonekana mhunzi ye yote katika nchi yote ya Israeli; kwa kuwa Wafilisti walisema, Waebrania wasije wakajifanyizia panga au mikuki; lakini Waisraeli wote hushuka kwa Wafilisti, ili kunoa kila mtu jembe lake, na mundu wake, na shoka lake, na sululu yake; ila walikuwa na tupa za kunolea sululu, na miundu, na mauma, na mashoka; na kwa kuinoa michokoo. Hivyo ikawa, siku ya vita, haukuonekana mkononi mwa mtu ye yote, miongoni mwa watu waliokuwa pamoja na Sauli na Yonathani, upanga wala mkuki; isipokuwa Sauli mwenyewe na mwanawe Yonathani walikuwa navyo.”

 

-          Daudi alikuwa na ufahamu kuwa vita ni ya Bwana, Daudi alikuwa na uelewa wa wazi kuwa wao walikuwa na silaha duni, na walinyimwa teknolojia na hata utengenezaji wa silaha za vita za chuma, watu waliokuwa na silaha katika Israel ni Sauli na mwanae Jonathani, hivyo Daudi aliweka tumaini lake lote kwa Mungu, alielewa kuwa kombeo ilikuwa ni silaha duni sana na haikuwa na mchango wowote kwa mtu ambaye amejivika vyuma mwili mzima lakini alielewa kuwa Mungu angekuwa nyuma ya kombeo na angeliongoza jiwe kupita popote palipo wazi hata kama ni kwenye jicho kwani alijifunza kuwa kombeo lililoongozwa na Bwana halitakosa kulenga shabaha, na mkuki na upanga kama Bwana hayuko navyo haziwezi kuwa silaha za kutisha kwake, watu waliojifunza kutumia kombeo au teo walikuwa na uwezo wa kuitumia kwa usahihi sana tangu nyakati za waamuzi watumiaji wa kombeo walikuwa wanauwezo wa kulenga hata unywele kwa jiwe  na wasikose shabaha kwa hiyo usahihi wa matumizi ya kombeo ulikuwa wa uhakika kwa kiwango cha juu, sana na kwa sababu hiyo Daudi hakuidharau silaha yake ndogo na duni akijua kuwa Mungu ataitumia  

 

1Samuel 17:45   Ndipo Daudi akamwambia yule Mfilisti, Wewe unanijia mimi na upanga, na fumo, na mkuki, bali mimi ninakujia wewe kwa jina la Bwana wa majeshi, Mungu wa majeshi ya Israeli uliowatukana.”

 

Waamuzi 20:14-16 “Lakini wana wa Benyamini wakakutanika huko Gibea kutoka katika miji yao, ili watoke kwenda kupiga vita juu ya wana wa Israeli. Hao wana wa Benyamini walihesabiwa siku ile kutoka hiyo miji, watu waume ishirini na sita elfu waliotumia upanga, zaidi ya hao waliokaa Gibea, ambao walihesabiwa watu wateule mia saba. Katika watu hao wote walikuwako watu waume mia saba waliochaguliwa, wenye shoto; kila mmoja alikuwa anaweza kuutupia unywele mawe kwa teo, wala asikose.”

 

Ni kutokana na umahiri wa silaha hii leo hii Idara ya ulinzi ya Israel Israel Defense Force (IDF) wameendeleza silaha ya kisasa kabisa inayoitwa kwa jina hili la kombel la Daudi “David’s Sling” ambayo ilianza kutumika kijeshi mwaka 2017 ikiwa na uwezo wa kuingilia kati na kuharibu mifumo ya ushambuliaji ya maadui kama wakitumia ndege, drones, na mabomu ya mashambulizi ya kisasa Ballistics missiles za uwezo wa aina mbalimbali kuanzia kilomita 40 mpaka 300 katika mifumo ya kivita ya kisasa ya israel      

Kanisa na kombeo la Daudi.

Mungu katika mpango wake hata leo bado ameendelea kulifundisha kanisa lake na kulihimiza, kuendelea kuweka tumaini letu kwake katika maeneo yote, Pamoja na maendeleo ya kitaaluma na teknolpojia iliyoko leo na mpanuko mkubwa wa elimu Bado Mungu anataka tumpe yeye kipaumbele na katika nguvu zake na hekima ya Mungu kuliko nyenzo za kisasa zilizoko duniani, kuhudumu kwetu na kufundisha kwetu na kuhubiri kwetu kamwe kusiangukie katika hekima ya kibinadamu bali tuendelee kuzitegemea nguvu za Mungu katika maisha yetu yote Paulo mtume alikuwa msomi, mwanasheria mkubwa na mwanafalsafa aliyebobea hata hivyo, alimtegemea sana Mungu katika huduma yake kuliko Elimu yake  na uwezo wake wa kushawishi, Mungu hutumia Imani  yetu katika jina lake na upako  hata kuliko vyeti vyetu vya kitaaluma, sio vibaya kuwa na taaluma lakini tusisahahu upako una sehemu muhimu katika maisha yetu ya huduma na utumishi, jumbe zangu zote zinatokana na muongozo wa Roho Mtakatifu kwanza kisha taaluma hufuata baadae katika maandalizi, lakini Mungu Roho Mtakakatifu ni namba moja kwangu.

1Wakorintho 2:4-5 “Na neno langu na kuhubiri kwangu hakukuwa kwa maneno ya hekima yenye kushawishi akili za watu, bali kwa dalili za Roho na za nguvu, ili imani yenu isiwe katika hekima ya wanadamu, bali katika nguvu za Mungu.”   

Paulo mtume alikuwa na ujuzi ya kuwa Mungu anaweza kuwatumia wenye cheo na wenye hekima ya dunia hii, lakini alitahadharisha kuwa Mungu huyatumia mambo manyonge na madhaifu na yaliyodharauliwa, na wadhaifu, kwa sababu Mungu hataki watu wajisifie mbele zake kwa sababu ya uwezo wa kibinadamu, bali kwaajili ya jina lake.

1Wakorintho 1:26-29 “Maana, ndugu zangu, angalieni mwito wenu, ya kwamba si wengi wenye hekima ya mwilini, si wengi wenye nguvu, si wengi wenye cheo walioitwa; bali Mungu aliyachagua mambo mapumbavu ya dunia awaaibishe wenye hekima; tena Mungu alivichagua vitu dhaifu vya dunia ili aviaibishe vyenye nguvu; tena Mungu alivichagua vitu vinyonge vya dunia na vilivyodharauliwa, naam, vitu ambavyo haviko, ili avibatilishe vile vilivyoko; mwenye mwili awaye yote asije akajisifu mbele za Mungu.”

Paulo alikuwa na ujuzi ya kuwa Mungu anaweza kumtumia mtu kwa rehema zake na neema yake tu na ya kuwa juhudi za kibinadamu haina mchango wowote katika kutupatia kibali cha Mungu, wala jitidaha za kibinadamu hazina mchango wa kuleta rehema za Mungu kwetu wala matakwa yetu

Warumi 9:10-16 “Wala si hivyo tu, lakini Rebeka naye, akiisha kuchukua mimba kwa mume mmoja, naye ni Isaka, baba yetu,(kwa maana kabla hawajazaliwa wale watoto, wala hawajatenda neno jema wala baya, ili lisimame kusudi la Mungu la kuchagua, si kwa sababu ya matendo, bali kwa sababu ya nia yake aitaye), aliambiwa hivi, Mkubwa atamtumikia mdogo. Kama ilivyoandikwa, Nimempenda Yakobo, bali Esau nimemchukia.Tuseme nini basi? Kuna udhalimu kwa Mungu? Hasha! Maana amwambia Musa, Nitamrehemu yeye nimrehemuye, nitamhurumia yeye nimhurumiaye. Basi, kama ni hivyo, si katika uwezo wa yule atakaye, wala wa yule apigaye mbio; bali wa yule arehemuye, yaani, Mungu.”

Neno la Mungu linatufundisha kuwa kuna namna ambapo Mungu asipohusika kwenye jambo lolote hata tujihusishe vipi jambo hilo haliwezi kuwa na maanikio bila ya mkono wake   na jambo hili ndio liko kwenye siri ya kombeo la Daudi           

Zaburi 127:1 “Bwana asipoijenga nyumba Waijengao wafanya kazi bure. Bwana asipoulinda mji Yeye aulindaye akesha bure.”  

Yohana 15:4-5 “Kaeni ndani yangu, nami ndani yenu. Kama vile tawi lisivyoweza kuzaa peke yake, lisipokaa ndani ya mzabibu; kadhalika nanyi, msipokaa ndani yangu. Mimi ni mzabibu; ninyi ni matawi, akaaye ndani yangu nami ndani yake, huyo huzaa sana; maana pasipo mimi ninyi hamwezi kufanya neno lo lote.”

Tunajifunza kuacha kuzitegemea Pesa kuliko Mungu kuingilia kati maswala yetu, kuacha kutegemea miundo mbinu bila kumruhusu Roho Mtakatifu katika shughuli zetu, kuacha kutegemea wingi wa watu kuliko uwepo wa Mungu, tulitegemee neno la Mungu kama upanga wa roho kwaajili ya ushindi katika maisha yetu, tuyategemee maombi yetu kuleta matokeo kuliko akili zetu na tumtegemee Mungu kwa Imani hata katika mambo madogo yasiyotatrajiwa, tutumie kile ambacho Mungu amekiweka ndani yetu kwa utukufu wake na tunataona ushindi mkubwa katika maisha yetu na hilo ndio kombeo la Daudi, Bila uwepo wa Mungu kombeo lisingeweza kuwa sababu ya ushindi wa Daudi.

 

Na Rev. Innocent Samuel Kamote

Mkuu wa wajenzi mwenye Hekima.

Jumapili, 15 Februari 2026

Sauti ya kijana huko jangwani!


Mwanzo 21:14-20 “Ibrahimu akaamka asubuhi na mapema akatwaa mkate na kiriba cha maji, akampa Hajiri akimtwika begani pake, na kijana, akamruhusu; naye akatoka, akapotea katika jangwa la Beer-sheba. Yale maji yakaisha katika kiriba, akamlaza kijana chini ya kijiti kimoja. Akaenda akakaa akimkabili, mbali naye kadiri ya mtupo wa mshale; maana alisema, Nisimwone kijana akifa; naye akakaa akimkabili, akapaza sauti yake, akalia. Mungu akasikia sauti ya kijana. Malaika wa Mungu akamwita Hajiri kutoka mbinguni, akamwambia, Una nini, Hajiri? Usiogope, maana Mungu amesikia sauti ya kijana huko aliko. Ondoka, ukamwinue kijana, ukamshike mkononi mwako, kwa kuwa nitamfanya kuwa taifa kubwa. Mungu akamfumbua macho, naye akaona kisima cha maji; akaenda akakijaza kiriba maji, akamnywesha kijana. Mungu akawa pamoja na huyo kijana, naye akakua, akakaa katika jangwa, akawa mpiga upinde.”




Utangulizi:

Kama kuna mojawapo ya matukio magumu sana duniani ni pamoja na tukio la kukataliwa na baba yako aliyekuzaa, maumivu ya kukataliwa na baba yanaweza kusababisha jeraha lisiloweza kukoma, hofu, kukosa kujiamini na kutelekezwa, jambo ambalo linaweza kupunguza kwa kiwango kikubwa uwezo wa kuwaamini watu, lakini pia linaweza kusababisha msongo wa mawazo, kushindwa kujitambua na kutokujitosheleza, inahitajika nguvu ya ziada sana kuweza kuwa kawaida na kuishinda hali ya kukataliwa, Lazima uwe na kitu cha ziada kuweza kujijenga kuwa unastahili na kujikomboa kutoka katika maumivu hayo ya kihisia kwani hali hii inazalisha hali ya kutaka  kujithibitisha.

Haya ndiyo yaliyomkuta Ishmael baada ya kufukuzwa nyumbani kwa baba yake ambaye kimsingi alikuwa tajiri sana wa mifugo fedha na dhahabu, lakini inaelezwa kuwa Ishamel na mama yake walitolewa mikono mitupu, wakipewa maji na mkate tu na hawakuwa hata na mtu wa kuwasindikiza, wala hawakuwa na chakula hata cha akiba, bali tupu.

Mwanzo 13:21-3 “Abramu akapanda kutoka Misri, yeye, na mkewe, na kila alichokuwa nacho, na Lutu pamoja naye, mpaka kusini. Naye Abramu alikuwa ni tajiri sana kwa mifugo, kwa fedha, na kwa dhahabu. Akaendelea kusafiri kutoka kusini mpaka Betheli, mahali pale palipokuwapo hema yake kwanza kati ya Betheli na Ai;”

Abrahamu alikuwa ni mtu aliyefanikiwa sana, alikuwa na makundi makubwa ya mifugo, wasimamizi, wafanyakazi, utajiri mkubwa wa fedha na dhahabu, lakini alikuwa ni mtu mwenye jeshi kali lililoweza kupigana vita na wafalme wakubwa katika vita, na moja ya vita maarufu aliyopigana na kuteka nyara ni vita iitwayo “opereshini Lutu”, ambapo alikwenda kupigana kumuokoa Lutu, Jeshi hilo lilikuwa na makomandoo 318 ambao walikuwa wamefunzwa vizuri  

Mwanzo 14:5-16 “Na mwaka wa kumi na nne akaja Kedorlaoma na wafalme waliokuwa pamoja naye, wakawapiga Warefai katika Ashteroth-karnaimu, na Wazuzi katika Hamu, na Waemi katika Shawe-kiryathaimu,na Wahori katika mlima wao Seiri, mpaka Elparani iliyo karibu na jangwa. Kisha wakarudi wakaja mpaka Enmisfati, ndio Kadeshi, wakapiga nchi yote ya Waamaleki, na Waamori waliokaa Hasason-tamari. Mfalme wa Sodoma, na mfalme wa Gomora, na mfalme wa Adma, na mfalme wa Seboimu, na mfalme wa Bela, ndio Soari, wakatoka wakapanga vita panapo bonde la Sidimu; wapigane na Kedorlaoma mfalme wa Elamu, na Tidali mfalme wa Goimu, na Amrafeli mfalme wa Shinari, na Arioko mfalme wa Elasari, wafalme wanne juu ya wale watano. Na bonde la Sidimu lilikuwa limejaa mashimo ya lami. Nao wafalme wa Sodoma na Gomora wakakimbia, wakaanguka huko, nao waliosalia wakakimbia milimani. Wakachukua mali zote za Sodoma na Gomora na vyakula vyao vyote, wakaenda zao. Wakamtwaa Lutu, mwana wa nduguye Abramu, aliyekaa huko Sodoma, na mali yake, wakaenda zao. Mtu mmoja aliyeponyoka akaenda, akampasha habari Abramu Mwebrania; naye amekaa panapo mialoni ya Mamre, yule Mwamori, ndugu ya Eshkoli, na ndugu ya Aneri, na hao walikuwa wamepatana na Abramu. Abramu aliposikia ya kwamba nduguye ametekwa mateka, akawapa silaha vijana wake, waliozaliwa katika nyumba yake, watu mia tatu na kumi na wanane, akawafuata mpaka Dani. Akajipanga apigane nao usiku, yeye na watumwa wake, akawapiga, akawafukuza mpaka Hoba, ulioko upande wa kushoto wa Dameski. Naye akarudisha mali zote, akamrudisha na Lutu nduguye na mali zake, na wanawake pia, na watu.”

Kwa hiyo unapata picha jinsi Abrahamu alivyokuwa mtu mkubwa sana mwenye uwezo mwingi na utajiri na mtu mwenye kumiliki Jeshi lake binafsi, na alipigana na wafalme zaidi ya watano na kuwashinda na kumrejesha Lutu na familia yake nyumbani na mifugo na mali zake sasa anamfukuza mtoto wa kumzaa mwenyewe tena mikono mitupu! Kwa mujibu wa  vitabu vya mafafanuzi ya kiyahudi na tamaduni zake viitwavyo “Talmudi” na “Midrashi” vinaeleza hivi kwa lugha ya kiingereza kuhusu Ishamel “Ishmael’s experience upon being sent away by Abraham was one of severe trauma, desperation and existential abandonment” kwa tafasiri yangu isiyo rasmi wanasema swala la kufukuzwa kwa Ishmael na Abrahimu lilikuwa ni mojawapo ya tukio baya, la kusikitisha, na kutelekezwa kikatili, kusikokuwa kwa kawaida” mtu tajiri mwenye uwezo mkubwa usiokuwa wa kawaida anamtoa mtoto wake wa kumzaa mikono mitupu bila kujali hali yake ya baadaye itakuwaje hata kama alizaliwa na mjakazi!

Mgogoro ulianza wakati Sara alipomshuhudia Ishmael akimdhihaki Isaka siku ile alipofanyiwa ibada ya shukurani kwaajili ya muujiza ule mkubwa wa kuzaliwa kwake Isaka na kuachishwa kunyonya

Mwanzo 21:6-10 “Sara akasema, Mungu amenifanyia kicheko; kila asikiaye atacheka pamoja nami. Akasema, N'nani angemwambia Ibrahimu, Sara atanyonyesha wana? Maana nimemzalia mwana katika uzee wake. Mtoto akakua, akaachishwa kunyonya; Ibrahimu akafanya karamu kuu siku ile Isaka alipoachishwa kunyonya. Sara akamwona yule mwana wa Hajiri Mmisri, ambaye alimzalia Ibrahimu, anafanya dhihaka. Kwa hiyo akamwambia Ibrahimu, Mfukuze mjakazi huyu na mwanawe, maana mwana wa mjakazi hatarithi pamoja na mwanangu, Isaka.”

Jambo hili halikumfurahisha Abraham, hata hivyo Mungu alimwambia Abrahamu afanye kile ambacho Sara ameagiza

Mwanzo 21:11.-12 “Na neno hilo lilikuwa baya sana machoni pa Ibrahimu, kwa ajili ya mwanawe. Mungu akamwambia Ibrahimu, Neno hili lisiwe baya machoni pako, kwa ajili ya huyo mwana, na huyo mjakazi wako. Kila akuambialo Sara, sikiza sauti yake, kwa maana katika Isaka uzao wako utaitwa.”

Jambo hili linamuweka Ishmael na mama yake katika wakati mbaya sana sasa wanapitia hali ngumu na ya uchungu sana, tutaliangalia somo hizi Sauti ya kijana Jangwani kwa kuzingatia vipengele vitatu vifuatavyo:-

·         Maumivu ya kukataliwa

·         Sauti ya kijana huko jangwani

·         Mungu anamkumbuka kijana huko jangwani

Maumivu ya kukataliwa

Tunawaona Ishmael na mama yake wakiwa jangwani maji yanawaishia na mkate unamalizika hali ya mauti sasa ndiyo inayomzunguka mtoto, akiwa ni kijana wa miaka 16 tu ambaye alilelewa maisha ya kudekezwa kama mtoto pekee nyumbani ghafla maisha yanabadilika na anatupwa jangwani, moyoni ana maumivu makali ya kutupwa na kukataliwa anajiona kama mtu asiye na bahati na ambaye amesalitiwa na baba yake na sio hivyo tu ametelekezwa, Ishmael na mama yake wanachanganyikiwa wamefukuzwa nyumbani nani kama wanatakiwa kuja kufia jangwani.

Mwanzo 21:14-16 “Ibrahimu akaamka asubuhi na mapema akatwaa mkate na kiriba cha maji, akampa Hajiri akimtwika begani pake, na kijana, akamruhusu; naye akatoka, akapotea katika jangwa la Beer-sheba. Yale maji yakaisha katika kiriba, akamlaza kijana chini ya kijiti kimoja. Akaenda akakaa akimkabili, mbali naye kadiri ya mtupo wa mshale; maana alisema, Nisimwone kijana akifa; naye akakaa akimkabili, akapaza sauti yake, akalia.”  

Maji yamekwisha chakula pia kimeisha ni jambo la kushangaza kuwa wanatupwa hata bila ya chakula cha akiba na wanapotelea katika jangwa anakabiliwa na kiu anachoka na wamekuwa dhaifu, mama yake anamuweka katika kichaka cha nyikani anakimbia mbali ili asimuone mtoto wake anapokata roho ana wasiwasi na hofu ya kuona mauti ikimmaliza mwanae

Kijana anajutia kumdhihaki Isaka anatambua kosa lake ambalo sasa linamletea mateso, anakuwa imara na anapokea mabadiliko toba yake inaonekana kwa ushahidi kuwa alimalizana vizuri na baba yake kwani alielewa upumbavu wake na sasa alimuheshimu Isaka kwa mujibu wa masimulizi ya marabi wa kiyahudi “Rabbinic tradition” (Genesis Rabbah) adhabu hii ilileta toba na mabadiliko makubwa kwani alikuja kumzika baba yake kwa heshima akiwa na Isaka ona:-

Mwanzo 25:8-10. “Ibrahimu akafariki, naye akafa katika uzee mwema, mzee sana, ameshiba siku, akakusanyika kwa watu wake. Isaka na Ishmaeli wanawe wakamzika katika pango ya Makpela, katika shamba la Efroni bin Sohari Mhiti, lielekealo Mamre. Katika lile shamba alilolinunua Ibrahimu kwa wazawa Hethi, huko ndiko alikozikwa Ibrahimu na Sara mkewe.”

Ndugu yangu kutelekezwa hakumaanishi kuwa umefika mwisho wa maisha, kutelekezwa hakumaanishi kuwa Mungu amemalizana na wewe watu wanaweza kukukataa na kukutelekeza lakini Mungu kamwe hawezi kufanya hivyo, Mikono yake bado iko wazi na anaweza kukupokea, Jangwa ndilo linalomfanya mtu kuwa imara na kuacha upumbavu wake, Jangwa lilikuwa eneo la somo kwa Ishmael, alijifunza kusamehe hakumuwekea kinyongo baba yake  Mungu aliisikiliza sauti yake kule jangwani  na alikuwa amemuandalia kisima kizuri cha maji ambayo yangeokoa uhai wake na kumfanya kuwa kijana shujaa,

Zaburi 34:6-9 “Maskini huyu aliita, Bwana akasikia, Akamwokoa na taabu zake zote.Malaika wa Bwana hufanya kituo, Akiwazungukia wamchao na kuwaokoa. Onjeni mwone ya kuwa Bwana yu mwema; Heri mtu yule anayemtumaini. Mcheni Bwana, enyi watakatifu wake, Yaani, wamchao hawahitaji kitu.”

Sauti ya kijana huko jangwani

Mwanzo 21:17-21 “Mungu akasikia sauti ya kijana. Malaika wa Mungu akamwita Hajiri kutoka mbinguni, akamwambia, Una nini, Hajiri? Usiogope, maana Mungu amesikia sauti ya kijana huko aliko. Ondoka, ukamwinue kijana, ukamshike mkononi mwako, kwa kuwa nitamfanya kuwa taifa kubwa. Mungu akamfumbua macho, naye akaona kisima cha maji; akaenda akakijaza kiriba maji, akamnywesha kijana. Mungu akawa pamoja na huyo kijana, naye akakua, akakaa katika jangwa, akawa mpiga upinde. Akakaa katika jangwa la Parani; mama yake akamtwalia mke katika nchi ya Misri.”

Jina Ishmael maana yake Mungu amesikia kilio changu, Mungu alisikia kilio cha mtoto, Mungu sio dhalimu hata pale inapoonekana kuwa ndoto zako zimezikwa na unabii kukuhusu umefukiwa katika mchanga, Mungu ataendelea kuwa mwaminifu kwa watu wake na neno lake mbingu ziliitikia sauti jangwani, kijana kweli alikuwa amefukuzwa nyumbani lakini hakuwa amefukuzwa kutoka kwenye uwepo wa Mungu, Mungu alimwambia Hajiri usiogope, na Mungu aliyafunua macho yake na akaona kisima chenye maji, kisima ambacho kimsingi kilikuwapo pale  tayari, watu wengi sio kuwa Mungu amewaacha bali watu wengi wamefungwa macho wasione fursa na ndio maana wanalia, Ni kazi ya Roho wa Mungu kukufunulia fursa, hauna sababu ya kulia lakini unapaswa kuinua macho yako uone.

Unaweza kukataliwa, kuteswa na kufukuzwa na hata kuwekwa nje ya mtandao “Systems” unaweza kutupwa na baba yako wa kiroho kabisa na unaweza usijaliwe na wale waliotakiwa kukujali lakini hili ndio tunalojifunza kuwa kama Mungu nanaweza kusikia kilio jangwani taabu yako haiwezi kunyamaziwa mbinguni, inaweza kunyamaziwa na wanadamu lakini Mungu hawezi kunyamaza, unaweza kufukuzwa, unaweza kuwa na kiu na unaweza hata kusahaulika , lakini Mungu hawezi kuacha kukusikia, utembeleo wa malaika hauzuiliki na hali, na uhakika wa maisha yako ya baadae uko mikononi mwa Mungu, maji yanaweza kuisha, mkate unaweza kumalizika, milango inaweza kufunga na watu wanaweza kukaa kimya lakini Mungu anayemsikiliza Ishmael yuko hata leo yeye hatakuacha ufie jangwani atakufunulia macho yako na atakuelekeza nini cha kufanya, Mungu alikuwa pamoja na Ishamel Mungu hana upendeleo haijalishi wewe ni wa mwanamke muungwana au wa mjakazi.

Mungu anamkumbuka kijana huko jangwani

Mungu alikumbuka agano lake alilolifanya na mama yake kuhusu kijana aliahidi kuwa angemfanya taifa kubwa na kwa sababu hiyo kufa jangwani haukuwa mpango wa Mungu, Mungu alikumbuka mpango wake na Mungu alisikia kilio cha Ishmael Mungu akamkumbuka kijana huko jangwani!

Mwanzo 16:6-11 “Naye Abramu akamwambia Sarai, Tazama, mjakazi wako yu mkononi mwako, mtendee lililo jema machoni pako. Sarai akamtesa, naye akakimbia kutoka mbele yake. Malaika wa BWANA akamwona kwenye chemchemi ya maji katika jangwa, chemchemi iliyoko katika njia ya kuendea Shuri. Akamwambia, Hajiri, wewe mjakazi wa Sarai, unatoka wapi, nawe unakwenda wapi? Akanena, Nakimbia mimi kutoka mbele ya bibi yangu Sarai. Malaika wa BWANA akamwambia, Rudi kwa bibi yako, ukanyenyekee chini ya mikono yake. Malaika wa BWANA akamwambia, Hakika nitauzidisha uzao wako, wala hautahesabika kwa jinsi utakavyokuwa mwingi. Malaika wa BWANA akamwambia, Tazama! Wewe una mimba, utazaa mwana wa kiume, nawe utamwita jina lake Ishmaeli, maana BWANA amesikia kilio cha mateso yako.”

Mungu alizungumza na Hajiri wakati wa changamoto, Mungu huleta ufumbuzi wakati wa changamoto, Mungu alimwambia asiogope, na Mungu alimfunulia macho kuona kisima cha maji, Mungu alikuwa ameahidi kumfanya Ishamel kuwa taifa kubwa na Ishamel akawa mkuu mno na wafalme 12 walitokea katika viuno vyake

Mwanzo 25:12-17 “Hivi ndivyo vizazi vya Ishmaeli, mwana wa Ibrahimu, ambaye Hajiri, Mmisri, mjakazi wa Sara, alimzalia Ibrahimu. Na haya ndiyo majina ya wana wa Ishmaeli, kwa majina yao, na kwa vizazi vyao. Mzaliwa wa kwanza wa Ishmaeli, ni Nebayothi, na Kedari, na Abdeeli, na Mibsamu, na Mishma, na Duma, na Masa, na Hadadi, na Tema, na Yeturi, na Nafishi, na Kedema. Hao ndio wana wa Ishmaeli, na hayo ni majina yao, katika miji yao, na katika vituo vyao, maseyidi kumi na wawili kwa kufuata jamaa zao. Na hii ndiyo miaka ya maisha ya Ishmaeli, miaka mia na thelathini na saba. Akakata roho, akafa, akakusanyika kwa watu wake.”

Mungu ndiye anayeshikilia maisha yako, mipango yako iko katika mikono yake tangu kuwekwa kwa misingi ya ulimwengu, hakuna bahati mbaya yeye ni muumba mwenye upendo, kila mtu duniani yuko katika mpango wake na ni yeye ndiye anayeziongoza njia zako, na makusudi yake kwako atayatimiza mwenyewe katika mpango wake haijalishi ni vikwazo gani utakutana navyo au ni giza gani liko mbele yako hiyo haimaanishi kuwa Mungu amekuacha ni swala la kufumba na kufumbua tu amini mchakato wa Mungu “trust the process” yeye atakulinda, atakuongoza atakuweka katika njia iliyo sahihi, hakuna anayeweza kuuzuia mpango wake wala makusudi yake, Mungu anaweza kuwainua watu kwaajili yako na wakakutendea mema watakusaidia kulifikia kusudi lako haijalishi watu wamekuchezea kiasi gani lakini Mungu ni mwenye nguvu kuliko wao, Je uko kwenye jangwa gani? Mungu anaisikia sauti yako, hutafia jangwani yeye bado hajamalizana na wewe, Mungu ana ahadi na wewe na ni lazima aitimize!

 

Na Rev. Innocent Samuel Kamote

 

Mkuu wa wajenzi mwenye Hekima 

Jumapili, 8 Februari 2026

Kanuni za kuwekea/kuwekewa Mikono:


Matendo 13:1-3Na huko Antiokia katika kanisa lililokuwako palikuwa na manabii na waalimu, nao ni Barnaba, na Simeoni aitwaye Nigeri, na Lukio Mkirene, na Manaeni aliyekuwa ndugu wa kunyonya wa mfalme Herode, na Sauli. Basi hawa walipokuwa wakimfanyia Bwana ibada na kufunga, Roho Mtakatifu akasema, Nitengeeni Barnaba na Sauli kwa kazi ile niliyowaitia. Ndipo wakiisha kufunga na kuomba, wakaweka mikono yao juu yao, wakawaacha waende zao.”




Utangulizi.

Leo nataka kuzungumzia mojawapo ya ibada ya muhimu na ya msingi na ya zamani sana, katika utamaduni wa kanisa na kimaandiko na hii ni ibada ya kuwekea mikono au kuwekewa mikono, Ibada hii ni ya muhimu kwa sababu ni ya kimaandiko na inaendelea kutenda kazi hata katika siku zetu, ingawa kuna umuhimu wa kujikumbusha ili tuweze kuwa na uelewa wa kina na mapana na marefu kuhusu kuwekea au kuwekewa mikono, kuwekea au kuwekewa mikono kuna uwezo wa kuruhusu neema ya Mungu juu ya maisha ya huduma na utumishi wa mtu, aidha pia mikono inahusika katika kupitisha Baraka, neema na uponyaji wa mwili nafsi na roho kwa hiyo uko umuhimu wa Kanisa kuwa na uelewa.

Kumbukumbu 34:9 “Na Yoshua, mwana wa Nuni, alikuwa amejaa roho ya hekima; maana Musa alikuwa amemwekea mikono yake juu yake; wana wa Israeli wakamsikiliza, wakafanya kama Bwana alivyomwamuru Musa.”

2Timotheo 1:6-7 “Kwa sababu hiyo nakukumbusha, uichochee karama ya Mungu, iliyo ndani yako kwa kuwekewa mikono yangu. Maana Mungu hakutupa roho ya woga, bali ya nguvu na ya upendo na ya moyo wa kiasi.”

Kwa msingi huu leo tutachukua muda kujifunza kwa kina na mapana na marefu kuhusu swala zima la kuwekea au kuwekewa mikono, ambalo kimsingi ni lazima liambatane na maombi kama ilivyo kwenye swala la kufunga, au kupaka mafuta vilevile kuweka mikono huendana na kuomba au kusema maneno yanayoambatana na kusudi la kuwekea mikono huko, ili kulitungua kusudi hilo kutoka katika ulimwengu wa roho na mkao wa Moyo kwa kusudi la kutimiza mapenzi ya Mungu, tutajifunza somo hili Kanuni za kuwekea au kuweka Mikono kwa kuzingatia vipengele vifuatavyo:-


·         Asili ya kuwekea au kuwekewa mikono.

·         Makusudi ya ibada ya kuwekea au kuwekewa mikono

·         Kanuni za kuwekea au kuwekewa mikono


Asili ya kuwekea au kuwekewa mikono.

Kuwekea mikono au kuwekewa mikono “laying on of hands” ni tendo la ibada la kimwili ambapo mtu au watu au kikundi cha watu huweka mikono inayoambatana na maombi juu ya wengine kama ishara ya kiroho yenye lengo la kubariki, kuhamisha mamlaka, kuweka wakfu viongozi, kuwatenga watu kwaajili ya huduma, kufanya maombezi ya uponyaji, kuchochea karama, kurithisha Baraka na kutambulisha na ubatizo wa Roho Mtakatifu, Tendo hili ingawa linafanyika katika mwili kiibada linaunganisha mamlaka ya Mungu ndani ya Mwanadamu anayepokea kusudi hilo. Ni ishara inayoonekana ya neema ya Mungu isiyoonekana na uweza wa Roho Mtakatifu.

Tendo la kuwekea mikono kwa asili linaonekana katika maandiko ya Kiebrania likitajwa kwa kiebrania kwa neno “Semikhah” kwa kiingereza “succession” kwa kiwahili ni kurithisha kwa mfululizo, mfano kutoka katika uongozi wa mtu mmoja kwenda katika uongozi wa mtu mwingine kwa kurithishana kwa Amani au kwa lengo la kuendeleza au kusaidia au kupitisha mfano Musa alipozidiwa na majukumu ya kichungaji katika kanisa lililokuwako Jangwani alichagua wazee sabini “70” kwa maelekezo ya Mungu na kuwawekea mikono na kwa tendo hilo sehemu ya utendaji wa Musa  iliwapata wazee wale sabini ili waweze kumsaidia majukumu yake.

Hesabu 11:24-29 “Musa akatoka, akawaambia watu maneno ya Bwana; akawakutanisha watu sabini miongoni mwa wazee wa watu, akawaweka kuizunguka Hema. Ndipo Bwana akashuka ndani ya wingu, akanena naye, akatwaa sehemu ya roho iliyokuwa juu ya Musa, akaitia juu ya wale wazee sabini; ikawa, roho hiyo ilipowashukia, wakatabiri, lakini hawakufanya hivyo tena. Lakini watu wawili walisalia kambini, jina la mmoja aliitwa Eldadi, na jina la wa pili aliitwa Medadi; na roho ile ikawashukia; nao walikuwa miongoni mwao walioandikwa, lakini walikuwa hawakutoka kwenda hemani; nao wakatabiri kambini. Mtu mmoja kijana akapiga mbio, akaenda akamwambia Musa, akasema, Eldadi na Medadi wanatoa unabii kambini. Yoshua mwana wa Nuni, mtumishi wa Musa tangu ujana wake, akajibu akasema, Ee bwana wangu Musa, uwakataze. Musa akamwambia, Je! Umekuwa na wivu kwa ajili yangu; ingekuwa heri kama watu wote wa Bwana wangekuwa manabii na kama Bwana angewatia roho yake.”

Hesabu 27:16-20 “Bwana, Mungu wa roho za wenye mwili wote, na aweke mtu juu ya mkutano, atakayetoka mbele yao, na kuingia mbele yao; atakayewaongoza watokapo, na kuwaleta ndani; ili mkutano wa Bwana wasiwe kama kondoo wasio na mchungaji. Bwana akamwambia Musa, Mtwae Yoshua, mwana wa Nuni, mtu mwenye roho ndani yake, ukamwekee mkono wako; kisha ukamweke mbele ya Eleazari kuhani, na mbele ya mkutano wote; ukampe mausia mbele ya macho yao. Nawe utaweka juu yake sehemu ya heshima yako, ili mkutano wote wa wana wa Israeli wapate kutii.”

Asili nyingine ya kuwekea mikono ilifanywa na makuhani kwa kuweka mikono yao juu ya mnyama kwaajili ya sadaka ya kuteteketezwa ya dhambi, Kuhani angeweka mikono yake juu ya mnyama kama ishara ya kusafirisha dhambi ya hatia kutoka kwa mwanadamu anayeombewa au kufanyiwa upatanishi kuelekea kwa mnyama huyo kisha angechinjwa na kuteketezwa kama ishara ya msamaha wa dhambi kutoka kwa muathirika, aidha tukio kama hili lilifanywa na kuhani mkuu kwaajili ya dhambi za taifa kwa mwanambuzi wa hazazeli mbuzi wa kafara ambaye angechukua uovu wa watu na kupotelea nao jangwani.

Walawi 1:2-5 “Nena na wana wa Israeli, uwaambie, Mtu wa kwenu atakapomtolea BWANA matoleo, mtatoa matoleo yenu katika wanyama wa mifugo, katika ng'ombe na katika kondoo. Matoleo yake kwamba ni sadaka ya kuteketezwa ya ng'ombe, atatoa ng'ombe mume mkamilifu; ataleta mlangoni pa hema ya kukutania, ili akubaliwe mbele ya BWANA. Kisha ataweka mkono wake juu ya kichwa cha hiyo sadaka ya kuteketezwa; nayo itakubaliwa kwa ajili yake, ili kufanya upatanisho kwa ajili yake. Naye atamchinja huyo ng'ombe mbele ya BWANA; kisha wana wa Haruni, hao makuhani, wataileta karibu hiyo damu, na kuinyunyiza damu yake kando-kando katika madhabahu iliyo hapo mlangoni pa hema ya kukutania.”

Walawi 16:21-22 “Na Haruni ataweka mikono yake miwili juu ya kichwa cha yule mbuzi aliye hai, na kuungama juu yake uovu wote wa wana wa Israeli, na makosa yao, naam, dhambi zao zote; naye ataziweka juu ya kichwa chake yule mbuzi, kisha atampeleka aende jangwani kwa mkono wa mtu aliye tayari.Na yule mbuzi atachukua juu yake uovu wao wote, mpaka nchi isiyo watu; naye atamwacha mbuzi jangwani.”

Asili nyingine ya tendo la kuwekea mikono ni kwaajili ya urithi au kuhamisha Baraka, ambapo tunaona Yakobo akiwarithi watoto wa Yusufu na kuwa wa kwake, huku akiweka mkono wa kuume juu ya mdogo na mkono wa kushoto juu ya mkubwa ili kumuinua Efraimu na kumshusha Manase katika mbaraka wake.

Mwanzo 48:13-16 “Yusufu akawaweka wote wawili, Efraimu katika mkono wake wa kuume, kuelekea mkono wa kushoto wa Israeli; na Manase katika mkono wake wa kushoto, kuelekea mkono wa kuume wa Israeli, akawasogeza karibu naye. Israeli akanyosha mkono wake wa kuume akauweka juu ya kichwa cha Efraimu, aliyekuwa mdogo, na mkono wake wa kushoto akauweka juu ya kichwa cha Manase, huku akijua atiavyo mikono; maana Manase ndiye aliyezaliwa kwanza. Akambariki Yusufu, akasema, Mungu ambaye baba zangu, Ibrahimu na Isaka, walienenda mbele zake, yeye Mungu aliyenilisha, maisha yangu yote, hata siku hii ya leo, naye Malaika aliyeniokoa na maovu yote, na awabariki vijana hawa; jina langu na litajwe juu yao, na jina la baba zangu, Ibrahimu na Isaka; na wawe wingi wa watu kati ya nchi.”

Ibada ya kuwekea mikono imekuwa na matumizi makubwa sana katika nyakati za agano jipya katika mazingira mbalimbali, Mwandishi wa kitabu cha Waebrania anayataja mafundisho ya msingi katika Kristo na mojawapo ya mafundisho haya ni pamoja na ibada za kuwekea mikono

Waebrania 6:1-3 “Kwa sababu hiyo, tukiacha kuyanena mafundisho ya kwanza ya Kristo, tukaze mwendo ili tuufikilie utimilifu; tusiweke msingi tena wa kuzitubia kazi zisizo na uhai, na wa kuwa na imani kwa Mungu, na wa mafundisho ya mabatizo, na kuwekea mikono, na kufufuliwa wafu, na hukumu ya milele. Na hayo tutafanya Mungu akitujalia.”

Makusudi ya ibada ya kuwekea au kuwekewa mikono.

Kwa ujumla unapolichunguza neno la Mungu kuhusu swala zima la kuwekea mikono utaweza kugundua kuwa ibada ya kuweka mikono au kuwekea mikono inafanyika kwa makusudi ya aina mbalimbali kama ifuatavyo:-

1.       Kwa kusudi la kubariki – Kimsingi moja ya sababu ya kuwekea mikono au kuwekewa mikono ni kwaajili ya Baraka za Mungu kwa yule anayewekewa mikono, Baraka za Mungu humfanya mtu awe na kibali na awe na mafanikio katika jambo analolifanya au analowekwa kulifanya kwaajili ya ufalme wa Mungu au kwa makusudi mengine, Mfano tunaona Yakobo akiweka mikono juu ya wajukuu zake ili kuwatakia Baraka za kinabii katika maisha yao, Lakini sio hivyo tu tunamuona bwana Yesu akiweka mikono juu ya watoto kwa kusudi la kuwabariki, aidha katika tamaduni za kikanisa pia watu wamekuwa wakiwawekea mikono wana ndoa wakati wa kuwatakia maisha mema katika ibada ya ndoa hili linaingia katika kundi hili la kuwekea mikono ili kuwabariki.

 

Mwanzo 48:20 “Akawabariki siku ile akasema, Katika ninyi Waisraeli watabariki, wakisema, Mungu na akufanye kama Efraimu na Manase. Akamweka Efraimu mbele ya Manase.”

 

Mathayo 19:13-15 “Ndipo akaletewa watoto wadogo ili aweke mikono yake juu yao na kuwaombea; wanafunzi wake wakawakemea. Lakini Yesu akasema, Waacheni watoto wadogo waje kwangu; wala msiwazuie; kwa maana walio mfano wa hao, ufalme wa mbinguni ni wao. Akaweka mikono yake juu yao, akatoka huko.”

 

Na kwa mujibu wa maelekezo ya kibiblia kama mtu atafanya ibada ya kubariki anayebariki anapaswa kuwa mkubwa kwa sababu Baraka hutoka kwa mkubwa kwenda kwa mdogo, kwa maana mtu huyo awe kuhani kwa maana ya mtumishi wa Mungu ambaye ni mkubwa kwa mamlaka aliyopewa na Mungu ya kubariki, lakini pia awe mkubwa kiumri, kwa hiyo ile mila ya kuwekewa mkono na mtoto mdogo kwa kuamini kuwa atakubariki ni kinyume na maelekezo ya kibiblia

 

Waebrania 7:1-7 “Kwa maana Melkizedeki huyo, mfalme wa Salemu, kuhani wa Mungu aliye juu, aliyekutana na Ibrahimu alipokuwa akirudi katika kuwapiga hao wafalme, akambariki; ambaye Ibrahimu alimgawia sehemu ya kumi ya vitu vyote; (tafsiri ya jina lake kwanza ni mfalme wa haki, tena, mfalme wa Salemu, maana yake, mfalme wa amani; hana baba, hana mama, hana wazazi, hana mwanzo wa siku zake, wala mwisho wa uhai wake, bali amefananishwa na Mwana wa Mungu); huyo adumu kuhani milele. Basi, angalieni jinsi mtu huyo alivyokuwa mkuu, ambaye Ibrahimu, baba yetu mkuu, alimpa sehemu ya kumi ya nyara. Na katika wana wa Lawi nao, wale waupatao ukuhani, wana amri kutwaa sehemu ya kumi kwa watu wao, yaani, ndugu zao, kwa agizo la sheria, ijapokuwa wametoka katika viuno vya Ibrahimu. Bali yeye, ambaye uzazi wake haukuhesabiwa kuwa umetoka kwa hao, alitwaa sehemu ya kumi kwa Ibrahimu, akambariki yeye aliye na ile ahadi. Wala haikanushiki kabisa kwamba mdogo hubarikiwa na mkubwa.”

 

2.       Kwa kusudi la kurithisha Uongozi – sababu nyingine ya ibada ya kuwekea mikono ni kwaajili ya kurithisha uongozi, “Semikhah” kwa kiingereza “succession hii hufanyika kwa kusudi la kumrithisha kiongozi kutoka kwa uongozi wa zamani kuja kwa uongozi mpya, wakati huu sehemu kama ile ya heshima au Roho yule yule aliyetenda kazi na kiongozi aliyepita hufanya kazi na kiongozi ajaye hata kama ni katika mtindo na mfumo wa aina nyingine na tabia nyingine lakini Roho ni yeye yule, Jambo hili linapofanyika sehemu ya heshima au mamlaka iliyokuweko juu ya kiongozi wa awali huamia kwa uongozi mpya na kumpa neema ya kutumika sawa na kiongozi wa awali au zaidi katika namna nyingine apendavyo Roho yeye yule.

 

Hesabu 27:16-20 “Bwana, Mungu wa roho za wenye mwili wote, na aweke mtu juu ya mkutano, atakayetoka mbele yao, na kuingia mbele yao; atakayewaongoza watokapo, na kuwaleta ndani; ili mkutano wa Bwana wasiwe kama kondoo wasio na mchungaji. Bwana akamwambia Musa, Mtwae Yoshua, mwana wa Nuni, mtu mwenye roho ndani yake, ukamwekee mkono wako; kisha ukamweke mbele ya Eleazari kuhani, na mbele ya mkutano wote; ukampe mausia mbele ya macho yao. Nawe utaweka juu yake sehemu ya heshima yako, ili mkutano wote wa wana wa Israeli wapate kutii.”

 

3.       Kwa kusudi la kuombea uponyaji na kufanya miujiza – Neno la Mungu linaonyesha kuwa ibada ya kuweka mikono pia inaweza kufanywa kwa nia ya kufanya maombezi na kuwaponya watu au kutumiwa na Mungu kwa njia ya miujiza, kwa hiyo utaweza kuona Yesu, na mitume kadhaa akiwemo Petro na Paulo na kadhalika ambao waliweza kuwaombea watu kwa kuwawekea mikono na wakapokea uponyaji, hata Yesu Kristo mwenyewe aliahidi ya kuwa wale wamuaminio watatumiwa kwa ishara mbalimbali ikiwa ni pamoja na kuweka mikono juu ya wagonjwa nao kupokea afya

 

Marko 6:4-5 “Yesu akawaambia, Nabii hakosi heshima, isipokuwa katika nchi yake mwenyewe, na kwa jamaa zake, na nyumbani mwake. Wala hakuweza kufanya mwujiza wo wote huko, isipokuwa aliweka mikono yake juu ya wagonjwa wachache, akawaponya.”

 

Matendo 9:11-12 “Bwana akamwambia, Simama, enenda zako katika njia iitwayo Nyofu, ukaulize katika nyumba ya Yuda mtu aitwaye Sauli, wa Tarso; maana, angalia, anaomba; naye amemwona mtu, jina lake Anania, akiingia, na kumwekea mikono juu yake, apate kuona tena.”

 

Matendo 28:7-8 “Karibu na mahali pale palikuwa na mashamba ya mkuu wa kisiwa, jina lake Publio; mtu huyu akatukaribisha kwa moyo wa urafiki, akatufanya wageni wake kwa muda wa siku tatu. Ikawa babaake Publio alikuwa hawezi homa na kuhara damu. Paulo akaingia kwake, akaomba, akaweka mikono yake juu yake, na kumpoza.”

 

Marko 16:17-18 “Na ishara hizi zitafuatana na hao waaminio; kwa jina langu watatoa pepo; watasema kwa lugha mpya; watashika nyoka; hata wakinywa kitu cha kufisha, hakitawadhuru kabisa; wataweka mikono yao juu ya wagonjwa, nao watapata afya.”

 

4.       Kwa kusudi la kumpokea Roho Mtakatifu – Uko ushahidi wa kimaandiko unaoshiria kuwa pamoja na kuweko kwa njia nyingi sana za watu kubatizwa kwa Roho Mtakatifu, inaonekana pia kuwa watu huweza kupokea Ubatizo wa Roho Mtakatifu kwa kuwekewa mikono  mfano

 

Matendo 8:14-19 “Na mitume waliokuwako Yerusalemu, waliposikia ya kwamba Samaria imelikubali neno la Mungu, wakawapelekea Petro na Yohana; ambao waliposhuka, wakawaombea wampokee Roho Mtakatifu; kwa maana bado hajawashukia hata mmoja wao, ila wamebatizwa tu kwa jina lake Bwana Yesu. Ndipo wakaweka mikono yao juu yao, nao wakampokea Roho Mtakatifu. Hata Simoni alipoona ya kuwa watu wanapewa Roho Mtakatifu kwa kuwekewa mikono ya mitume, akataka kuwapa fedha akisema, Nipeni na mimi uwezo huu, ili kila mtu nitakayemweka mikono yangu, apokee Roho Mtakatifu.”

 

Matendo 19:1-6 “Ikawa, Apolo alipokuwa Korintho, Paulo, akiisha kupita kati ya nchi za juu, akafika Efeso; akakutana na wanafunzi kadha wa kadha huko; akawauliza, Je! Mlipokea Roho Mtakatifu mlipoamini? Wakamjibu, La, hata kusikia kwamba kuna Roho Mtakatifu hatukusikia. Akawauliza, Basi mlibatizwa kwa ubatizo gani? Wakasema, Kwa ubatizo wa Yohana. Paulo akasema, Yohana alibatiza kwa ubatizo wa toba, akiwaambia watu wamwamini yeye atakayekuja nyuma yake, yaani, Yesu. Waliposikia haya wakabatizwa kwa jina la Bwana Yesu. Na Paulo, alipokwisha kuweka mikono yake juu yao, Roho Mtakatifu akaja juu yao; wakaanza kunena kwa lugha, na kutabiri.”

 

5.       Kwa kusudi la kuchochewa kwa karama – Wakati mwingine watu wa Mungu huwa na karama za Roho Mtakatifu ndani yao na vipawa mbalimbali lakini wakati mwingine karama zina tabia ya kujificha na hivyo mtu anaweza kuwekewa mikono na karama zikachochewa, tunapoendelea kumtumikia Mungu kama ilivyokuwa kwa Timotheo kwa muda Fulani wakati mwingine kuna uwezekano wa moto kupungua kutokana na changamoto mbalimbali Paulo alimtaka Timotheo ili kumuwekea mikono yake ili karama ziendelee kuwaka na kufanyakazi kwa kiwango cha juu Zaidi, karama pia huweza kuambukizwa ndani ya Mtu kwa kuwekewa mikono.

 

2Timotheo 1:6-7 “Kwa sababu hiyo nakukumbusha, uichochee karama ya Mungu, iliyo ndani yako kwa kuwekewa mikono yangu. Maana Mungu hakutupa roho ya woga, bali ya nguvu na ya upendo na ya moyo wa kiasi.”

 

1Timotheo 4:13-14 “Hata nitakapokuja, ufanye bidii katika kusoma na kuonya na kufundisha. Usiache kuitumia karama ile iliyomo ndani yako, uliyopewa kwa unabii na kwa kuwekewa mikono ya wazee.”

 

6.       Kwa kusudi la kusimika au kuweka wakfu viongozi wa kanisa na wale walioitwa katika wito maalumu – Viongozi wote makanisani wanapokuwa wameteuliwa au kuchaguliwa kwaajili ya kutimiza majukumu yao kadhaa waliyoitiwa na Roho Mtakatifu katika kanisa wanapaswa kuwekewa mikono ili wapokee neema ya kuwawezesha kubeba majukumu yao ya kikanisa au ya kitumishi kwa hiyo nyakati za kanisa la Kwanza kila walipoweka viongozi waliwawekea mikono.

 

Matendo 6:5-6 “Neno hili likapendeza machoni pa mkutano wote; wakamchagua Stefano, mtu aliyejaa imani na Roho Mtakatifu, na Filipo, na Prokoro, na Nikanori, na Timoni, na Parmena, na Nikolao mwongofu wa Antiokia; ambao wakawaweka mbele ya mitume, na walipokwisha kuomba wakaweka mikono yao juu yao.”

 

Matendo 13:1-3 “Na huko Antiokia katika kanisa lililokuwako palikuwa na manabii na waalimu, nao ni Barnaba, na Simeoni aitwaye Nigeri, na Lukio Mkirene, na Manaeni aliyekuwa ndugu wa kunyonya wa mfalme Herode, na Sauli. Basi hawa walipokuwa wakimfanyia Bwana ibada na kufunga, Roho Mtakatifu akasema, Nitengeeni Barnaba na Sauli kwa kazi ile niliyowaitia.Ndipo wakiisha kufunga na kuomba, wakaweka mikono yao juu yao, wakawaacha waende zao.”

 

7.       Huwezi kupokea roho chafu kwa kuwekewa mikono – Kumekuwepo na hofu kubwa sana kutoka kwa washirika na hata  baadhi ya watumishi wa Mungu mbali mbali wakionya kuwa uko uwezekano wa kupokea roho chafu kutokana na kuwekewa mikono, ni muhimu kufahamu kuwa Mkrito aliyeokoka vizuri na aliye muaminifu hawezi kamwe kupokea roho chafu kwa kuwekewa mikono  na mhudumu asiye mwaminifu, Mkristo aliyeokoka vema na kujazwa Roho Mtakatifu yeye ni Hekalu la Roho Mtakatifu na Roho wa Mungu anakaa ndani yake  

 

1Wakorintho 6:19 “Au hamjui ya kuwa mwili wenu ni hekalu la Roho Mtakatifu aliye ndani yenu, mliyepewa na Mungu? Wala ninyi si mali yenu wenyewe;”

 

Roho wa Mungu aliye ndani ya waamini au watu waliookoka ni mkuu kuliko yeye aliyeko katika ulimwengu huu kwa hiyo utabarikiwa na kufanikiwa kwa sababu ya tendo la kiungu na ibada inayofanyika ndani yako na sio kwa sababu ya hali ya mtumishi anayekuwekea mikono

 

1Yohana 4:4 “Ninyi, watoto wadogo, mwatokana na Mungu nanyi mmewashinda, kwa sababu yeye aliye ndani yenu ni mkuu kuliko yeye aliye katika dunia.”  

 

Yesu anaonyesha katika maandiko na mafundisho yake kuwa Mwamini hupewa kile anachokiomba na Mungu sio dhalimu kwamba akupe nyoka wakati umeomba samaki, au nge wakati umeomba yai na jiwe wakati umeomba Mkate Mungu huangalia moyo na atakupa sawasawa na uhitaji wa moyo wako na sio kwa sababu ya hali ya muhubiri au kiongozi anayekuwekea mikono

 

Luka 11:9-13 “Nami nawaambia, Ombeni, nanyi mtapewa; tafuteni, nanyi mtaona; bisheni, nanyi mtafunguliwa. Kwa kuwa kila aombaye hupokea; naye atafutaye huona; naye abishaye atafunguliwa. Maana ni yupi kwenu aliye baba, ambaye mwanawe akimwomba mkate, atampa jiwe au samaki, badala ya samaki atampa nyoka? Au akimwomba yai, atampa nge? Basi, ikiwa ninyi mlio waovu mnajua kuwapa watoto wenu vipawa vyema, je! Baba aliye mbinguni hatazidi sana kuwapa Roho Mtakatifu hao wamwombao?

 

Hana alipata mtoto katika wakati ambao watoto wa Eli yule kuhani walikuwa wameharibika na neno la Bwana lilikuwa adimu lakini kupitia maneno ya Eli na uhitaji wa mwanamke yule moyoni Mungu alijibu maombi nyake sawasawa na uhitaji wake kiyume kabisa na hali ya kuhani nyumbani mwa Bwana kwa hiyo hali ya kuhani sio changamoto ya kumfanya mtu asipokee kitu halisi anachikitamani na kukihitaji kutoka kwa Mungu.                        

 

Kanuni za kuwekea au kuwekewa mikono

Kama utakuwa umefuatilia vema somo hili utagundua kuwa kuweka mikono ni swala la kiroho na la Muhimu na kwa sababu hiyo lina kanuni zake, haliwezi kufanyika hovyo hovyo ama bila kufuata utaratibu na maelekezo ya kibiblia, kuwekea watu mikono ni njia ya kuruhusu neema ya Mungu kutoka kwa Roho Mtakatifu kupitia mikono yetu na kutimiza kusudi lake kwa mtu anayewekewa Mikono kwa hiyo tukio hili kama ilivyo kwa tukio la kupaka mafuta ni lazima lifanyike pamoja na maombi. Lakini pia kwa kuzingatia kanuni, kila anayeweka mikono ni lazima awe anajua anachokifanya na kujiuliza kwa nini anafanya na kusudi la kufanya hivyo, hivyo jambo hili lisifanyike ilimradi tu kwani ni ibada kamili.

Anayeweka mikono ni lazima awe anajua anachokifanya – Mtu anayeweka mikono anatakiwa awe anajua ni kwa nini anafanya hivyo, hili ni swala la kiroho na ni swala la maisha ni swala la kuinua mtu na kushusha mtu kwa hiyo anayeweka mikono anatakiwa kuwa na ujuzi na kile anachikifanya kwanza akiwa na ufahamu wa kawaida lakini pia kama ameongozwa na Mungu au roho ya kinabii kufanya hivyo ni lazima aelewe kusudi  linalomuongoza katika kuwekea mikono, Kwa mfano wakati Yakobo anamuwekea mkono wa kuume Efraimu na mkono wa kushoto Manase wakati Manase ndiye mkubwa na Efraimu ndiye mdogo, Yusufu alikuwa akielewa na kufikiri kuwa babaye anakosea lakini Yakobo alisisitiza kuwa anajua anachokifanya ona kumbe muwekewa mikono anapaswa kujua anachokifanya

Mwanzo 48:13-19 “Yusufu akawaweka wote wawili, Efraimu katika mkono wake wa kuume, kuelekea mkono wa kushoto wa Israeli; na Manase katika mkono wake wa kushoto, kuelekea mkono wa kuume wa Israeli, akawasogeza karibu naye. Israeli akanyosha mkono wake wa kuume akauweka juu ya kichwa cha Efraimu, aliyekuwa mdogo, na mkono wake wa kushoto akauweka juu ya kichwa cha Manase, HUKU AKIJUA ATIAVYO MIKONO; maana Manase ndiye aliyezaliwa kwanza. Akambariki Yusufu, akasema, Mungu ambaye baba zangu, Ibrahimu na Isaka, walienenda mbele zake, yeye Mungu aliyenilisha, maisha yangu yote, hata siku hii ya leo, naye Malaika aliyeniokoa na maovu yote, na awabariki vijana hawa; jina langu na litajwe juu yao, na jina la baba zangu, Ibrahimu na Isaka; na wawe wingi wa watu kati ya nchi. Yusufu alipoona kwamba babaye anaweka mkono wake wa kuume juu ya kichwa cha Efraimu, ikawa vibaya machoni pake. Akauinua mkono wa babaye auondoe katika kichwa cha Efraimu, ili auweke juu ya kichwa cha Manase. Yusufu akamwambia babaye, Sivyo, babangu, maana huyu ni mzaliwa wa kwanza; weka mkono wako wa kuume kichwani pake. Babaye akakataa, akasema, NAJUA, MWANANGU NAJUA, yeye naye atakuwa taifa, yeye naye atakuwa mkuu; lakini ndugu yake mdogo atakuwa mkubwa kuliko yeye, na uzao wake watakuwa wingi wa mataifa.”

Unaona utagundua katika kifungu hiki kuwa Yusufu na Yakobo walikuwa wanajua kuwa anayewekewa mikono wakati wa Baraka ikiwa atawezewa mkono wa kuume huyu ndiye atakuwa mkubwa na anayewekewa mkono wa kushoto atakuwa mdogo, hii ni kanuni ya kibiblia ambayo watumishi wengi wa Mungu huikosea hasa wakati wa kubariki maharusi kwa mfano unakuta wanaweka mikono hovyo na wakati mwingine mke anawekewa mkono wa kuume na mume anawekewa mkono wa kushoto hili ni kosa kubwa la kiufundi na kosa katika kanuni ya kuwekea mikono muweka mikono ni lazima awe anajua anachikifanya NAJUA MWANANGU NAJUA, HUKU AKIJUA ATIAVYO MIKONO je unajua jinsi ya kuweka mikono au unaweka tu? Sio hivyo tu jua kuwa sasa naweka mikono kwaajili ya uponyaji, au naweka mikono kwaajili ya kuchochea karama, au naweka mikono kwaajili ya kuweka kiongozi na kadhalika na wakati wote lile kusudi la kuweka mikono litatamkwa kwa maombi (kunuizia), unapoweka mikono kusimika kiongozi muwekee mkono wa kuume sio wa kushoto, shikiwa maiki na mtu kisha tumia mikono yako yute miwili muwekee mikono kiongozi mkuu, unakuta mtu ameshima maiki kwa mkono wa kulia anaweka wakfu kiongozi akitumia mkono wa kushoto na watu wote wanakodoa macho na kuona tukio hilo kama tukio la kawaida inaumiza sana watu kukosea kanuni za kuwekewa watu mikono!, Yusufu aliumia alipoona Manase anawekewa mkono wa kushoto kwa nini kwa sababu alitambua kimsingi kanuni hii

Kuweka au kuwekea mikono ni urithi wa kiroho – Katika ulimwengu wa roho tendo la kumuwekea mtu mikono ni tendo la kurithi, au kurithisha tunajifunza kuwa wakati Yakobo anaweka mikono juu ya Manase na Efraimu hawa walikuwa wajukuu wake lakini kitendo cha kuwawekea mikono kilibadilisha mfumo wa maisha ya Manase na Efraimu kutoka kuwa wajukuu zake na kuwa watoto wake sawa kabisa na Simeoni na Reuben  ona

Mwanzo 48:3-6 “Yakobo akamwambia Yusufu, Mungu Mwenyezi alinitokea huko Luzu, katika nchi ya Kanaani, akanibariki, akaniambia, Mimi hapa, nitakuongezea uzao wako, na kukuzidisha, nami nitakufanya uwe kundi la mataifa; kisha nitawapa wazao wako nchi hii baada yako, iwe milki ya milele. Basi sasa wanao wawili uliozaliwa katika nchi ya Misri kabla sijaja kwako Misri ni watoto wangu, yaani, Efraimu na Manase watakuwa wangu, kama Reubeni na Simeoni. Na wazao wako utakaozaa baada ya hawa watakuwa wako; kwa jina la ndugu zao wataitwa katika urithi wao.”

Hii maana yake ni nini anayeweka mikono anawarithi anaowawekea mikono kuwa wanaye na wanaowekewa mikono wanamrithi anayewawekea mikono kuwa baba yao nadhani ni katika dhana kama hii kumekuwa na hofu kwa watu wengi kuogopa kuwekewa mikono na kila mtu kwa kuhofia kuwa baba wa mtu ambaye humjui vema au kuwarithi watoto usiowafahamu vema kwa kuwa katika ulimwengu wa roho mnabadilishana DNA za kimamlaka na uongozi

Kuwekea mtu mikono ni kumuidhinisha au kumtambulisha – Tendo la kuwekea mtu mikono ni tendo la kumuidhinisha au kumtambulisha mtu kihuduma au kumuweka katika mamlaka ya uongozi, unamuweka mtu wakfu kwaajili ua huduma aliyoteuliwa au kuchaguliwa kuifanya kama ushemasi, umisheni na kadhalika kwa hiyo kitendo cha kumuwekea mikono ni utambuzi wa hadharani kuhusu aina ya wito aliyoitiwa anayewekea mikono au kuchochea karama au kuhamishia karama na mamlaka kumuwezesha mtu huyo kutumikia vema kusudi alilowekewa  na ndio maana bado Biblia inatoa tahadhari kuwa na umakini na unayemuwekea mikono ili kama ni mwovu kumuwekea mikono maana yake ni kushiriki kazi zake mbovu au kushiriki uovu kwa hiyo lazima unayemuwekea mikono uwe umemthibitisha kuwa hatakuaibisha

1Timotheo 5:21-22 “Nakuagiza mbele za Mungu, na mbele za Kristo Yesu, na mbele za malaika wateule, uyatende hayo pasipo kuhukumu kwa haraka; usifanye neno lo lote kwa upendeleo. Usimwekee mtu mikono kwa haraka, wala usizishiriki dhambi za watu wengine. Ujilinde nafsi yako uwe safi.”      

Unapomuwekea mtu mikono kwaajili ya huduma maana yake unagonga muhuri wako na kumuidhinisha mtu huyo katika huduma ile aliyoitiwa sasa endapo mtu huyu hayuko sawa maana yake kushindwa kwake kunawakilisha kushindwa kwako, wekea mikono mtu anayekuwakilisha vema, ambaye umemfunza vema  

Kuwekea mikono ni njia ya kupitisha neema ya Mungu.- tendo la kuwekea mikono kama ilivyo tendo la kupaka mafuta yote ni matendo ya kuipitisha neema ya Mungu kupitia mikono yetu kwenda kwa wengine kwa hiyo ni lazima tendo hili litumike pamoja na Maombi, kama ni kwaajili ya mgonjwa kutakuwa na dua maalumu kwajili ya mgonjwa kama ni kwaajili ya kuweka wakfu kiongozi dua itatamkwa ya kuweka wakfu kwa viongozi wanaohisika na waliokidhi vigezo

Yakobo 5:14-15 “Mtu wa kwenu amekuwa hawezi? Na awaite wazee wa kanisa; nao wamwombee, na kumpaka mafuta kwa jina la Bwana. Na kule kuomba kwa imani kutamwokoa mgonjwa yule, na Bwana atamwinua; hata ikiwa amefanya dhambi, atasamehewa.”

Matendo 15:40-41 “Lakini Paulo akamchagua Sila, akaondoka, akiombewa na wale ndugu apewe neema ya Bwana. Akapita katika Shamu na Kilikia akiyathibitisha makanisa.”

Kwa hiyo ibada zote za kuwekea mikono iwe ni kwaajili ya uponyaji, kubariki ndoa kuweka viongozi zote maana yake ni kuruhusu neema ya Mungu ipite juu ya wahusika na kuwawezesha katika wajibu unaohusika kwa hiyo ni lazima maombi yahusike kwa sababu hiyo kuwekea mikono sio uchawi ni njia ya kupitisha neema ya Mungu kwa hiyo kuwekea mikono ni njia inayoonekana ya kupitisha mambo yasiyoonekana ya kiungu kwenda kwa watu husika, kwa umaalumu wake kwa kanisa na ulimwengu lakini mwenye kutoa Baraka hizo ni Mungu mwenyewe, wakati wa kubariki watoto tunaweza kuwawekea mikono, wakati wa kubatiza tunaweza kumuwekea mtu mikono na kumuombea neema ya maisha ya uchaji wa Mungu na utumishi, wakati wa kuombea wagonjwa tunaweza kuwaombea wagonjwa neema ya kupokea uponyaji, wakati wa kubariki maharusi tunaweza kuwaombea maharusi neema na wakati wa kuweka wakfu viongozi mashemasi, makasisi, maaskofu na kadhalika na hata wakati wa kusimika askofu na viongozi mbalimbali ni vema wakawekewa mikono kuwaombea neema ya Mungu kisha Mungu mwenyewe atafanya kazi yake pamoja na watu wake kwa makusudi yaliyokusudiwa, kumbuka wakati wa kuwekea maharusi mikono ya Baraka weka mkono wa kuume kwa mume na mkono wa kushoto kwa mke kufanya kinyume na hayo ni kutengeneza migogoro ya kiroho na kimaongozi kwani Mungu hadhihakiwi waweka mikono lazima wajue nini wanachokifanya wakati wanaweka mikono. Ikiwa kanisa linaweka mikono kwa askofu mkuu, na askofu mkuu aliyekuwepo madarakani hayuko, askofu mkuu mteule atawekewa mikono na mtu mwenye mamlaka ya askofu mkuu aliyetsaafu au wa kanisa lingine, ama kutoka kwa wamishionari waanzilishi wa kanisa husika au mtu mwenye mamlaka ya huduma ya kitume.

Na. Rev. Innocent Samuel Kamote

Mkuu wa wajenzi mwenye Hekima