Wakolosai 1:9-11 “Kwa
sababu hiyo sisi nasi, tangu siku ile tuliposikia, hatuachi kufanya maombi na
dua kwa ajili yenu, ili mjazwe maarifa ya mapenzi yake katika hekima yote na
ufahamu wa rohoni; MWENENDE KAMA ULIVYO WAJIBU WENU KWA BWANA, mkimpendeza
kabisa; mkizaa matunda kwa kila kazi njema, na kuzidi katika maarifa ya Mungu;
mkiwezeshwa kwa uwezo wote, kwa kadiri ya nguvu ya utukufu wake, mpate kuwa na
saburi ya kila namna na uvumilivu pamoja na furaha; mkimshukuru Baba, aliyewastahilisha kupokea sehemu ya urithi wa
watakatifu katika nuru.”
Utangulizi:
Ni muhimu kufahamu kuwa
mara baada ya kuwa tumeokolewa kwa neema ya Mungu, kwa njia ya imani, tunapaswa
sana kuzingatia mwenendo wetu, Mtu aliyeokoka hataishi maisha anayojitakia tu
kwa sababu ameokolewa, Lakini maandiko yanatoa maelekezo ya jinsi tunavyopaswa
kuishi, yaani uko wajibu wetu tunaopaswa kutembea katika huo ili tuweze kuwa
mfano wa kuigwa kama wana wa Mungu tuwapo hapa ulimwenguni, mwenendo huo ni wa
lazima na wala sio wa hiyari, tunapaswa kuendenda kama vile Yesu Kristo
mwenyewe alivyoenenda hapa duniani.
1Yohana 2:4-6 “Yeye
asemaye, Nimemjua, wala hazishiki amri zake, ni mwongo, wala kweli haimo ndani
yake. Lakini yeye alishikaye neno lake, katika huyo upendo wa Mungu umekamilika
kweli kweli. Katika hili twajua ya kuwa tumo ndani yake. Yeye asemaye ya kuwa
anakaa ndani yake, imempasa KUENENDA mwenyewe vile vile kama yeye ALIVYOENENDA.”
Katika maandiko yetu ya
Msingi Paulo mtume anawaandikia Wakolosai aina ya maombi anayowaombea na
kuwalekeza watu hao wajazwe maarifa ya mapenzi yake katika hekima yote na
ufahamu wa rohoni ili kwamba waenende kama ulivyo wajibu wao kwa Bwana
wakimpendeza yeye Kabisa!, Kumbe tunagundua ya kuwa kuna namna basi Wakristo
tunapaswa kuenenda na swala hili liko wazi kabisa katika neno la Mungu. Kuna
namna ya kutembea katika ulimwengu huu
Wafilipi 2:14-15 “Yatendeni
mambo yote pasipo manung'uniko wala mashindano, mpate kuwa wana wa Mungu wasio
na lawama, wala udanganyifu, wasio na ila kati ya kizazi chenye ukaidi,
kilichopotoka; ambao kati ya hao mnaonekana kuwa kama mianga katika ulimwengu,”
Tito 2:11-12 “Maana
neema ya Mungu iwaokoayo wanadamu wote imefunuliwa; nayo yatufundisha kukataa
ubaya na tamaa za kidunia; tupate kuishi kwa kiasi, na haki, na utauwa, katika
ulimwengu huu wa sasa;”
Wakolosai 2:4-6 “Nasema
neno hili, mtu asije akawadanganya kwa maneno ya kuwashawishi. Maana nijapokuwa
sipo kwa mwili, lakini nipo pamoja nanyi kwa roho, nikifurahi na kuuona
utaratibu wenu na uthabiti wa imani yenu katika Kristo. Basi kama mlivyompokea
Kristo Yesu, Bwana, ENENDENI vivyo hivyo katika yeye;”
Kwa msingi huo utaweza
kuona kuwa maandiko matakatifu yana namna ambayo kwamba Roho Mtakatifu
ametukusudia sisi kuenenda sawasawa na maelekezo yanayotolewa katika maandiko lakini
ili tuweze kuendelea kuelewa vizuri hatuna budi kufahamu maswala kadhaa ikiwa
ni pamoja na maana ya neno mwenendo, tutajifunza somo hili Mwenende kama
ulivyo wajibu wenu kwa Bwana! Kwa kuzingatia vipengele muhimu vitatu
vifuatavyo;-
·
Maana ya
neno mwenendo.
·
Jinsi
inavyotupasa kuenenda.
·
Mwenende
kama ulivyo wajibu wenu kwa Bwana!
Maana ya neno mwenendo.
Neno mwenendo ambalo
limejitokeza zaidi ya mara 13 katika maandiko ya Kiyunani linasomeka kama
“AnastrophÄ“” ambalo katika Biblia ya kiingereza linasomeka kama “conversation”,
au “Behavior” au “Conducts” Katika Biblia ya Kiswahili limetumika
neno mawazo, au mtazamo, tabia au mwenendo
kwa mfano kabla ya kuokoka mtu anaweza kuwa na tabia au mwenendo ua mawazo yanayomuongoza kuwa na tabia hiyo,
kwa hiyo mwenendo ni jumla ya mtazamo wa mtu na mazingira yanayopelekea awe na
tabia hiyo aliyo nayo, Paulo mtume kabla ya kuokoka alikuwa na mtazamo kuwa
Ukristo sio imani ya kweli na kwa sababu hiyo aliwatesa sana Wakristo na kanisa
la kwanza kwa sababu mtazamo wake ulipelekea kuwa na mwenendo au tabia
aliyokuwa nayo kabla ya kukutana na Bwana Yesu.
Wagalatia 1:13 “Maana
mmesikia habari za MWENENDO wangu zamani katika dini ya Kiyahudi, kwamba
naliliudhi kanisa la Mungu kupita kiasi, nikaliharibu. Nami naliendelea katika
dini ya Kiyahudi kuliko wengi walio hirimu zangu katika kabila yangu,
nikajitahidi sana katika kuyashika mapokeo ya baba zangu. Lakini Mungu,
aliyenitenga tangu tumboni mwa mama yangu, akaniita kwa neema yake,”
Kwa hiyo mtu aliyeokoka
anapaswa kuwa na mabadiliko ya mwenendo wake wa kwanza au ule wa zamani na
anapaswa kuvaa mwenendo mpya unaotembea katika hali ya uchaji wa Mungu kwa
kuzingatia kweli, haki na utakatifu, kwa sababu hiyo mtu aliyemwamini Bwana
anatarajiwa awe na mwenendo tofauti na ule aliokuwa akiuendea zamani, haya ni
mabadiliko yanayoanzia kwemye mtazamo, fundisho na kuonekana katika tabia na
mtazamo mpya unaompa Mungu utukufu baada ya kumpokea Yesu kama Bwana na mwokozi
wa maisha yetu!
Waefeso 4:20-24 “Bali
ninyi, sivyo mlivyojifunza Kristo; ikiwa mlimsikia mkafundishwa katika yeye,
kama kweli ilivyo katika Yesu, mvue kwa habari ya MWENENDO wa kwanza utu wa
zamani, unaoharibika kwa kuzifuata tamaa zenye kudanganya; na mfanywe wapya
katika roho ya nia zenu; mkavae utu mpya, ulioumbwa kwa namna ya Mungu katika
haki na utakatifu wa kweli.”
Jinsi inavyotupasa kuenenda.
Tumejifunza sasa maana ya
mwenendo na tumeona jinsi maandiko yanavyotuelezea kuwa uko mwenendo ambao
tuliuendea zamani kabla ya kuokolewa na sasa baada ya kuwa tumeokolewa kuna
aina ya mwenendo ambao tunapaswa kuuenenda na bila kufundishwa wakati mwingine
inaweza kuwa ngumu kwetu kujua ni mwenendo gani tunapaswa kuufuata? Kwa hiyo
yako mambo kadhaa ambayo Biblia inatuasa kuyafuata au kuyajifunza ili yaweze
kuwa dira na njia ya kuujenga mwenendo wetu na huo ndio wajibu wetu ambao
umesisitizwa katika maandiko ya msingi kwamba Mwenende kama ulivyo wajibu wenu
kwa Bwana ni wajibu upi huo hapa yako mambo kadhaa ya kuyaangalia
1.
Ni wajibu wetu
kuenenda kwa utakatifu – Utakatifu ni moja ya mwenendo ambao watu waliookoka wanapaswa kuwa
nao, ni muhimu kuelewa kuwa ni vigumu kumuona Mungu bila ya kuwa na mwenendo wa
utakatifu, utakatifu ni nini hasa? Biblia ya Kiyunani inatumia neno “Hagio”
ambalo ni sawa na neno la Kiingereza “Pure morally” au “Blameless” maana yake kuendenda kwa uadilifu, au
kutembea bila lawama, wakati wote katika maisha yetu isitokee tumelaumiwa kama
watu wabaya au kwa kutenda mambo yasiyo ya uadilifu
1Petro 1:14-16. “Kama watoto wa kutii msijifananishe na tamaa zenu za
kwanza za ujinga wenu; bali kama yeye aliyewaita alivyo mtakatifu, ninyi nanyi
iweni watakatifu katika MWENENDO wenu wote; kwa maana imeandikwa, Mtakuwa
watakatifu kwa kuwa mimi ni mtakatifu.”
2.
Ni wajibu
wetu kuendenda kwa imani – watu wa Mungu wanapaswa kuenenda kwa Imani, pasipo imani haiwezekani
kumpendeza Mungu, kwa hiyo yote tuyatendayo tunapaswa kuyafanya kwa imani,
Mungu aliwaangamiza wana wa Israel wengi jangwani kwa sababu ya kutokuamini
kwao, tukiendenda kwa imani ni rahisi kumpendeza Mungu, watu wa Mungu wanapaswa
kuliamini neno la Mungu na kulitii kwa imani na sio kwa kutegemea yale
tuyaonayo kwa macho ya kibinadamu au mazingira yanayokuzunguka
2Wakorintho 5:6-8 “Basi siku zote tuna moyo mkuu; tena twajua ya kuwa,
wakati tuwapo hapa katika mwili, tunakaa mbali na Bwana. (Maana TWAENENDA kwa
imani, si kwa kuona.) Lakini tuna moyo mkuu; nasi tunaona ni afadhali
kutokuwamo katika mwili na kukaa pamoja na Bwana.”
3.
Ni wajibu
wetu kuenenda kwa Upendo – Kuenenda kwa upendo ni mojawapo ya agizo la watu wa Mungu, kuishi kwa
upendo, kutembea kwa upendo kujawa na upendo maisha yetu ni lazima yaonyeshe
upendo wa kujitoa kama vile Kristo alivyojitoa kwetu na kwa ulimwengu ili kila
amuaminiye aokolewe, chuki, husuda na wivu, magombano, visasi na majungu kamwe
sio mwenendo wanaopaswa kuwa nao watu ambao Kristo amewafia Msalabani kwa kujitoa
kuliko kukuu hata tulipokuwa wenye dhambi
Waefeso 5:1-2 “Hivyo mfuateni Mungu, kama watoto wanaopendwa; MKAENENDE
katika upendo, kama Kristo naye alivyowapenda ninyi tena akajitoa kwa ajili
yetu, sadaka na dhabihu kwa Mungu, kuwa harufu ya manukato.”
4.
Ni wajibu
wetu kuenenda nuruni – Kuenenda nuruni kwa ufupi maana yake ni kutembea kwa kuweka kipaumbele
maswala na maagizo ya Mungu, Mungu ni Nuru, Yesu Kristo mwenyewe pia alisema
yeye ni Nuru ya ulimwengu, kwa sababu hiyo tunapoweka kipaumbele maswala Yote
ambayo Yesu Kristo ametufundisha na kumfuata, maana yake tunaendenda Nuruni,
kwenda kinyume na maagizo ya neno la Mungu ni kuenenda gizani
1Yohana 1:5-7 “Na hii ndiyo habari tuliyoisikia kwake, na kuihubiri
kwenu, ya kwamba Mungu ni nuru, wala giza lo lote hamna ndani yake.Tukisema ya
kwamba twashirikiana naye, tena tukienenda gizani, twasema uongo, wala
hatuifanyi iliyo kweli; bali TUKIENENDA NURUNI, kama yeye alivyo katika nuru,
twashirikiana sisi kwa sisi, na damu yake Yesu, Mwana wake, yatusafisha dhambi
yote.”
5.
Ni wajibu
wetu kuenenda katika upya wa maisha – kutembea katika upya wa maisha kunamaanisha ni lazima maisha yetu
yabadilike tuwe na mwenendo mpya na sio ule wa zamani, kabala ya kuokolewa,
hatupaswi tena kuitumikia dhambi ambayo tuliiendea zamani kabla ya kukutana na
Yesu, sasa kwa kuwa tumekutana na Yesu hatuna budi kuenenda katika upya huu wa
maisha na kutembea na Mungu, uongo, ulevi, tamaa mbaya, uchafu, kiburi,
masengenyo, ubinafsi na kujihesabia haki pamoja na maovu ya kila namna
hayapaswi kuonekana tena kwa mtu anayewajibika kuenenda katika upya wa maisha
Warumi 6:4-6 “Basi tulizikwa pamoja naye kwa njia ya ubatizo katika
mauti yake, kusudi kama Kristo alivyofufuka katika wafu kwa njia ya utukufu wa
Baba, vivyo hivyo na sisi TUENENDE KATIKA UPYA WA UZIMA. Kwa maana kama
mlivyounganika naye katika mfano wa mauti yake, kadhalika mtaunganika kwa mfano
wa kufufuka kwake; mkijua neno hili, ya kuwa utu wetu wa kale ulisulibishwa
pamoja naye, ili mwili wa dhambi ubatilike, tusitumikie dhambi tena;”
6.
Ni wajibu
wetu kuenenda kwa Roho – kuenenda kwa Roho maana yake ni nini? Ni maisha ambayo Roho Mtakatifu
ndiye anayetawala, kila mtu aliyeokolewa ni muhimu na lazima atoe nafasi na
kumruhusu Roho Mtakatifu kuyaongoza na kuyatawala maisha yake katika kila nyanja
ya maisha na kumruhusu yeye kutusaidia kukomaa kiroho na kuzaa matunda ya Roho
Mtakatifu katika maisha yetu, maisha yako unayaongoza wewe mwenyewe au
unamuachia Roho akuongoze? Kuenenda kwa roho ni kumuachia yeye atuongoze maisha
yetu.
Wagalatia 5:16-23 “Basi nasema, ENENDENI kwa Roho, wala hamtazitimiza kamwe
tamaa za mwili. Kwa sababu mwili hutamani ukishindana na Roho, na Roho
kushindana na mwili; kwa maana hizi zimepingana, hata hamwezi kufanya
mnayotaka. Lakini mkiongozwa na Roho, hampo chini ya sheria. Basi matendo ya mwili
ni dhahiri, ndiyo haya, uasherati, uchafu, ufisadi, ibada ya sanamu, uchawi,
uadui, ugomvi, wivu, hasira, fitina, faraka, uzushi, husuda, ulevi, ulafi, na
mambo yanayofanana na hayo, katika hayo nawaambia mapema, kama nilivyokwisha
kuwaambia, ya kwamba watu watendao mambo ya jinsi hiyo hawataurithi ufalme wa
Mungu. Lakini tunda la Roho ni upendo, furaha, amani, uvumilivu, utu wema,
fadhili, uaminifu, upole, kiasi; juu ya mambo kama hayo hakuna sheria.”
7.
Ni wajibu
wetu kuenenda kama unavyostahili wito wetu – Kila mtu aliyeokolewa kuna namna Mungu amemuita amtumikie katika
mazingira mbalimbali na huo ndio wito wako, hapa wito haimaanishi ule wito wa
kumtumikia Mungu pekee, wito maalumu, unaweza kuwa Mwalimu, Polisi, Daktrari,
Mtoza ushuru, Mwanasiasa na kadhalika Mungu anataka uwe na mwenendo mwema
katika kila aina ya wito ulioitiwa au kokote kule unakokuweko hata kama wewe ni
fundi cherehani, iko miiko ya utumishi katika kile eneo la wito wa maisha basi
huko enenda kama unavyoustahili wito wako, zaidi sana katika nyumba ya Mungu huku tukitunza amani.
Waefeso 4:1-3
“Kwa hiyo nawasihi,
mimi niliye mfungwa katika Bwana, MWENENDE kama inavyoustahili wito wenu
mlioitiwa; kwa unyenyekevu wote na upole, kwa uvumilivu, mkichukuliana katika
upendo; na kujitahidi kuuhifadhi umoja wa Roho katika kifungo cha amani.”
8.
Ni wajibu
wetu kuenenda kwa Hekima – Ni kama maandiko yanatuambaia wazi kuwa muda wetu duniani sio wa kwetu ni
muda wa Mungu, Ni muda ambao tumepewa kwa kusudi la kumtumikia Mungu na
kutimiza kusudi lake au mapenzi yake kwa hiyo Muda ni wa maana sana kwa watu
waliookoka na haupaswi kupotezwa bure, watu wanaopoteza muda wanaitwa wasio na
hekima au wajinga, ni lazima tujiangalie tunautumiaje Muda hasa sisi waafrika,
tunaweza kutumia muda mwingi sana kupiga soga ua kusengenya muda ambao
tungeweza kuutumia kwaajili ya Mungu, kwa kuyajua mapenzi yake na kuyafanya
Waefeso 5:15-17 “Basi angalieni sana jinsi MNAVYOENENDA; si kama watu
wasio na hekima bali kama watu wenye hekima; mkiukomboa wakati kwa maana zamani
hizi ni za uovu. Kwa sababu hiyo msiwe wajinga, bali mfahamu ni nini yaliyo
mapenzi ya Bwana.”
9.
Ni wajibu
wetu kuenenda vilevile kama tulivyompokea Kristo – Kuenenda vile vile kama tulivyompokea Kristo
hakumaanishi ubaki vilevile baada ya kuokoka, lakini maana yake kila siku
tunapaswa kuishi vile vile sawasawa na mafundisho tunayoyapokea kwa Bwana wetu
Yesu Kristo kupitia Mwalimu wa Kweli Roho Mtakatifu, huku ni kuendelea
kudumisha uhusiano wetu na Mungu kwa kutii na kujileta katika neema yake kukua
katika upendo, unyenyekevu na hekima na kuhakikisha kuwa haturudi nyuma tangu
tulipoanza uhusiano wetu na yeye.
Wakolosai 2:6-7 “Basi kama mlivyompokea Kristo Yesu, Bwana, ENENDENI vivyo
hivyo katika yeye; wenye shina na wenye kujengwa katika yeye; mmefanywa imara
kwa imani, kama mlivyofundishwa; mkizidi kutoa shukrani.”
10.
Ni wajibu
wetu kuenenda kwa kuikulia neema – Tumeokolewa kwa neema sisi kama wana wa Mungu ni wana wa neema kwa msingi
huo hatuna budi kukua kwa kuikulia neema ya Mungu ni neema ya Mungu ndiyo
inayotusaidia katika, kuukulia wokovu na kukomaa kiroho kwa hiyo hatuna budi
kujitoa sisi wenyewe na kuenenda kwa kuikulia neema kwa kuendelea kutenda mema
Waefeso 2:8-10 “Kwa maana mmeokolewa kwa neema, kwa njia ya imani; ambayo
hiyo haikutokana na nafsi zenu, ni kipawa cha Mungu; wala si kwa matendo, mtu
awaye yote asije akajisifu. Maana tu kazi yake, tuliumbwa katika Kristo Yesu,
tutende matendo mema, ambayo tokea awali Mungu aliyatengeneza ili TUENENDE NAYO.”
Mwenende kama ulivyo wajibu wenu kwa Bwana!
Wokovu ni Msaada wa Mungu
kwetu, hata hivyo tabia na mwenendo ni wajibu wetu na ndio maana neno la Mungu
linasema mwenende kama ulivyo wajibu wenu kwa Bwana, ni wajibu wetu kujitoa kwa
Mungu na kukubali neema ya Mungu ituendeshe katika maisha haya kama watoto wake
uili tuweze kuwa na mvuto hapa ulimwenguni, mwenendo wetu una nafasi kubwa
mbili, kuimarisha uhusiano wetu wa ndani na Mungu, na pili kuwavutia wengine au
kuwafundisha kivitendo jinsi Mungu alivyo mwadilifu, kuenenda kama ulivyo
wajibu wetu kwa Bwana kumpa Mungu heshima inayoonyesha kuwa Mungu anabadilisha maisha ya watu wake, tunaweza kuitangaza
injili hata bila kusema neno kupitia tu mwenendo mwema, aina binadamu wote
duniani wanajua kiwango cha uadilifu ambao watu wa Mungu wanapaswa kuenenda na
ndio maana ukifanya mambo ya ajabu wanajua, kutokana na umuhimu wa jambo hili
Paulo mtume aliwaombea sana wakolosai wajazwe maarifa, na hekima na ufahamu wa
rohoni ili waenende kama ulivyo wajibu wao kwa Bwana wakimpendeza kabisa sio
hivyo tu wakiwavutia watu wengine wasioamini waweze kuokolewa ili hayo yatimie
hatuna budi kujitoa na kuhakikisha vile vile tunajileta wenyewe kanisani katika
ibada za mafundisho ili tukutane na neno la Mungu litakalotupoa hekima na
maarifa ili tujue nemna inavyotupasa kuenenda
Wakolosai 1:9-11 “Kwa
sababu hiyo sisi nasi, tangu siku ile tuliposikia, hatuachi kufanya maombi na
dua kwa ajili yenu, ili mjazwe maarifa ya mapenzi yake katika hekima yote na
ufahamu wa rohoni; MWENENDE KAMA ULIVYO WAJIBU WENU KWA BWANA, mkimpendeza kabisa;
mkizaa matunda kwa kila kazi njema, na kuzidi katika maarifa ya Mungu;
mkiwezeshwa kwa uwezo wote, kwa kadiri ya nguvu ya utukufu wake, mpate kuwa na
saburi ya kila namna na uvumilivu pamoja na furaha; mkimshukuru Baba, aliyewastahilisha kupokea sehemu ya urithi wa
watakatifu katika nuru.”
1Petro 3:1-2 “Kadhalika
ninyi wake, watiini waume zenu; kusudi, ikiwa wako wasioliamini Neno, wavutwe
kwa MWENENDO wa wake zao, pasipo lile Neno; wakiutazama MWENENDO wenu safi, na
wa hofu.”
Mwenendo ni msingi muhimu
sana katika maisha ya Ukristo, ni lazima kila Mkristo awe na mwenendo
unaomuakisi Yesu Kristo na hii ni kanuni Muhimu sana katika maisha ya ukristo
na mwenendo wa kibiblia, mwenendo mwema mbele ya watu wasiomjua Mungu huwavutia
watu wengine wapate kuokolewa, na sio hivyo tu ni mwenendo ndio unaotusaidia
kupata viongozi wa kanisa ambao mfano wao unaweza kuigizwa na wengine mwenendo
unatajwa kama hekima na tabia nzuri, unatajwa kama utetezi tunaposingiziwa,
unaonyesha kielelelzo kama viongozi katika nyumba ya Mungu kwa hivyo
tukiwajibika vizuri kwa Bwana tutawavutia watu kukubali ukweli ya kuwa Mungu
anaokoa na anabadilisha watu wake kwa sababu watu wataona mabadiliko makubwa ya
mwenendo wetu.
Yakobo 3:11-13. “Je!
Chemchemi katika jicho moja hutoa maji matamu na maji machungu? Ndugu zangu,
Je! Mtini waweza kuzaa zeituni, au mzabibu kuzaa tini? Kadhalika chemchemi
haiwezi kutoa maji ya chumvi na maji matamu. N'nani aliye na hekima na ufahamu
kwenu? Na aonyeshe kazi zake kwa MWENENDO wake mzuri, katika upole wa hekima.”
1Timotheo 4:12 “Mtu
awaye yote asiudharau ujana wako, bali uwe kielelezo kwao waaminio, katika
usemi na MWENENDO, na katika upendo na imani na usafi.”
1Petro 2:12 “Mwe na
MWENENDO mzuri kati ya Mataifa, ili, iwapo huwasingizia kuwa watenda mabaya,
wayatazamapo matendo yenu mazuri, wamtukuze Mungu siku ya kujiliwa.”
Na Rev. Innocent Samuel Kamote
Mkuu wa wajenzi mwenye Hekima


.jpg)