Jumapili, 31 Mei 2026

Nguvu ya kuomba kwa kupiga magoti!


Waefeso 3:14-17 “Kwa hiyo NAMPIGIA BABA MAGOTI, ambaye kwa jina lake ubaba wote wa mbinguni na wa duniani unaitwa, awajalieni, kwa kadiri ya utajiri wa utukufu wake, kufanywa imara kwa nguvu, kwa kazi ya Roho wake katika utu wa ndani. Kristo akae mioyoni mwenu kwa imani mkiwa na shina na msingi katika upendo;”



Utangulizi:

Wote tunafahamu kuwa maombi ni moja ya njia ya muhimu inayotumiwa na watu wengi sana katika kuunganisha ulimwengu wa roho na mwanadamu, tunaweza kusema kuwa maombi ndio pumzi ya uhai wa kila anayeamini, maombi yana nguvu, maombi yanaweza kuombwa kwa staili, mikao na mitindo mbalimbali inayotajwa pia katika maandiko, kwa mfano kufumba macho, au kufumbua, kusimama au kukaa, kuinua mikono au kukunja, kulala kifudifudi, au kuketi kimya, kuomba kwa sauti au kimya, laniki pia kuna kuomba kwa kupiga magoti, hata hivyo pamoja na kuwa mwanadamu anaweza kumuomba Mungu kwa mitindo mbalimbali leo nataka kuzungumzia swala la kuomba kwa kupiga magoti, watu wengi wanataka kuomba maombi yenye matokeo, yenye nguvu, lakini hawajui njia, Neno la Mungu linazungumzia maombi ya kupiga magoti kwa njia na namna ya kipekee sana kuna nguvu ya ziada wakati mwanadamu anapomuomba Mungu au kumuabudu Mungu huku akiwa amepiga magoti.

Luka 22:39-43 “Akatoka akaenda mpaka mlima wa Mizeituni kama ilivyokuwa desturi yake; wanafunzi wake nao wakafuatana naye. Alipofika mahali pale aliwaambia, Ombeni kwamba msiingie majaribuni. Mwenyewe akajitenga nao kama kiasi cha kutupa jiwe, AKAPIGA MAGOTI AKAOMBA, akisema, Ee Baba, ikiwa ni mapenzi yako, uniondolee kikombe hiki; walakini si mapenzi yangu, bali yako yatendeke. Malaika kutoka mbinguni akamtokea akamtia nguvu.”

Kumbe kuna matokeo katika maombi ya kupiga magoti,Kwa msingi huo basi leo tutachukua muda kujifunza kwa kina na mapana na marefu somo hili Nguvu ya kuomba kwa kupiga magoti kwa kuzingatia vipengele vitatu vifuatavyo:-

·         Maana ya kupiga magoti kimaandiko.

·         Mifano ya watu walioomba kwa kupiga magoti.

·         Nguvu ya kuomba kwa kupiga magoti.

Maana ya kupiga magoti kimaandiko.

Neno kupiga magoti katika lugha ya Kiebrania linatumika kama neno “Barak” na kwa Kiyunani  linatumika neno “Gonypeteo” Neno “Barak” la Kiebrania maana yake ni Kupiga magoti, au kuonyesha unyenyekevu, kuonyesha heshima au kujishusha mbele ya mtu unayemuheshimu, mtu mkubwa au Mungu, kwa hiyo kwa ujumla wake kupiga magoti maana yake ni tendo la kuonyesha unyenyekevu mbele za Mungu, kutambua ukuu wake  na kukubali kuwa wewe na mimi tunamtegemea Mungu, kwa hiyo kupiga magoti ni tendo linalotakiwa kuanzia moyoni na kujitokeza kwa nje katika jinsi ya mwili, Neno la Mungu linatoa  wito wa kumuabudu  kwa kumsujudia na kwa kumpigia magoti Mungu wetu, Kumbuka imeandikwa utamwabudu na kumsujudia Bwana Mungu wake peke yake!

Zaburi 95:6-7 “Njoni, tuabudu, tusujudu, TUPIGE MAGOTI MBELE ZA BWANA aliyetuumba. Kwa maana ndiye Mungu wetu, Na sisi tu watu wa malisho yake, Na kondoo za mkono wake. Ingekuwa heri leo msikie sauti yake!

Kupiga magoti au goti katika Lugha ya Kiyunani linatumika neno “Gonypeteo” ambalo ni muunganiko wa maneno mawili ya kiyunani yaani “Gonu” na “Pipto”.  “Gonu” ikiwa na maana ya Goti na “Pipto” ikiwa na maana ya anguka au kuanguka kwa kiingereza “fall on Knee” au “Kneel down” au “Bow the knee” Hili ni tendo la kuonyesha, unyenyekevu na utii, au kukubali kuwa chini ya maelekezo ya Mungu, ni njia inayotumika katika maombi hususani nyakati za agano jipya kuonyesha heshima kwa Yesu Kristo, lakini ni ishara ya kuonyesha kuwa una hitaji la muhimu na zito na linalohitaji msaada wa haraka au kupewa kipaumbele cha aina yake.

Mathayo 17:14-18 “Nao walipoufikia mkutano, mtu mmoja akamjia, AKAMPIGIA MAGOTI, akisema, Bwana, umrehemu mwanangu, kwa kuwa ana kifafa, na kuteswa vibaya; maana mara nyingi huanguka motoni, na mara nyingi majini. Nikamleta kwa wanafunzi wako, wasiweze kumponya. Yesu akajibu, akasema, Enyi kizazi kisichoamini, kilichopotoka, nitakaa pamoja nanyi hata lini? Nitachukuliana nanyi hata lini? Mleteni huku kwangu. Yesu akamkemea pepo, naye akamtoka; yule kijana akapona tangu saa ile.”

Kupiga magoti ni heshima kubwa na ni tendo la nje linalotoka moyoni lenye kuonyesha kuwa unakubali kunyenyekea kwa mwenye mamlaka, Maandiko yanaonyesha na kutabiri kuwa kwa Yesu Kristo kutokana na mamlaka kubwa sana aliyopewa kila goti la vitu vyote iwe ni mbinguni au duniani litapigwa kwake kwa sababu ya heshima kubwa aliyotunukiwa na Mungu Baba yake ona:-

Wafilipi 2:9-11 “Kwa hiyo tena Mungu alimwadhimisha mno, akamkirimia Jina lile lipitalo kila jina; ILI KWA JINA LA YESU KILA GOTI LIPIGWE, la vitu vya mbinguni, na vya duniani, na vya chini ya nchi; na kila ulimi ukiri ya kuwa YESU KRISTO NI BWANA, kwa utukufu wa Mungu Baba.”

Mifano ya watu walioomba kwa kupiga magoti.

Neno la Mungu limejaa mifano kadhaa ya watu kadhaa wa kadha ambao waliomba kwa kupiga magoti na kupata matokeo makubwa sana katika maombi yao, kimsingi kabla ya kuangalia nguvu ya maombi ya kupiga magoti au umuhimu wa maombi ya kupiga magoti eneo hili linatuonyesha moja kwa moja matokeo nguvu na umuhimu wa kupiga magoti wakati wa kuomba.

1.       Yesu Kristo -  Alipokuwa katika wakati mgumu sana kibinamu wa kukabiliwa na mauti ya msalaba  na mateso yaliyojaa dhihaka na kuvunjiwa heshima kwa kuwa alitambua ni mauti ya aina gani na mateso ya aina gani yalikuwa yanamkabili, moyo wake na hisia zake zilijawa na maumivu makali ya kupita kawaida, alikuwa na wakati mgumu alikuwa na wakati wa vita kali ya kiroho, wakati huu alitumia maombi ya kupiga magoti na mbingu zilimtia nguvu kwani alitumiwa malaika kutoka mbinguni mara moja ili kumtia nguvu ona!

 

Luka 22:39-43. “Akatoka akaenda mpaka mlima wa Mizeituni kama ilivyokuwa desturi yake; wanafunzi wake nao wakafuatana naye. Alipofika mahali pale aliwaambia, Ombeni kwamba msiingie majaribuni. Mwenyewe akajitenga nao kama kiasi cha kutupa jiwe, AKAPIGA MAGOTI AKAOMBA, akisema, Ee Baba, ikiwa ni mapenzi yako, uniondolee kikombe hiki; walakini si mapenzi yangu, bali yako yatendeke. Malaika kutoka mbinguni akamtokea akamtia nguvu.”

 

Ukichunguza kwa kina tukio hili utagundua ya kuwa maombi ya kupiga magoti yanafaa sana wakati mwanadamu akiwa katika shinikizo zito na hali ngumu kihisia na mambo ya kutisha yanapokukabili au unapokuwa na vita kubwa, wakati huo utahitaji kujinyenyekeza zaidi kwa kupiga magoti lakini pia unaweza kuona matokeo ya kupiga magoti kwani Malaika wa Bwana kutoka mbinguni alimtokea na kumtia nguvu.

 

2.       Daniel – Kulikuwa na mswada mkali wa kiserikali uliopitishwa kukataza watu kuomba kwa mungu yoyote kwa muda wa mwezi mmoja na mtu ambaye angekiuka swala hilo angetupwa katika tundu la simba wakali wenye njaa, tunamuona Daniel hakubadilisha kabisa mfumo wa maisha yake ya maombi  na hata katika wakati huu wa sheria kali kiasi hicho la tishio la maisha na kifo kwa simba wakali aliendelea kuomba kwa kupiga magoti mara tatu kila siku akiwa mwaminifu kwa Mungu wake na matokeo yanaonekana simba hawakumuweza, Mungu aliwatuma malaika wake wakayafunga makanwa ya simba na hawakumdhuru.

 

Daniel 6:6-11 “Basi wale mawaziri na maamiri wakakusanyika pamoja mbele ya mfalme, wakamwambia hivi, Mfalme Dario, uishi milele.  Mawaziri wote wa ufalme, na manaibu, na maamiri, na madiwani, na maliwali wamefanya shauri pamoja ili kuweka amri ya kifalme; na kupiga marufuku, ya kwamba mtu ye yote atakayeomba dua kwa Mungu awaye yote, au kwa mtu awaye yote, katika muda wa siku thelathini, ila kwako, Ee mfalme atatupwa katika tundu la simba. Sasa, Ee mfalme, piga marufuku, ukatie sahihi maandiko haya, yasibadilike, kama ilivyo sheria ya Wamedi na Waajemi, isiyoweza kubadilika. Basi mfalme Dario akayatia sahihi maandiko yale, na ile marufuku. Hata Danieli, alipojua ya kuwa yale maandiko yamekwisha kutiwa sahihi, akaingia nyumbani mwake, (na madirisha katika chumba chake yalikuwa yamefunguliwa kukabili Yerusalemu;) AKAPIGA MAGOTI MARA TATU KILA SIKU, AKASALI, akashukuru mbele za Mungu wake, kama alivyokuwa akifanya tokea hapo. Basi watu hao wakakusanyika pamoja, wakamwona Danieli akiomba dua, na kusihi mbele za Mungu wake.”

 

Daniel 6:19-24 “Asubuhi mfalme akaondoka mapema, akaenda kwa haraka mpaka penye lile tundu la simba. Naye alipolikaribia lile tundu, akamlilia Danieli kwa sauti ya huzuni; mfalme akanena; akamwambia Danieli, Ee Danieli, mtumishi wa Mungu aliye hai, je! Mungu wako, unayemtumikia daima, aweza kukuponya na simba hawa? Ndipo Danieli akamwambia mfalme, Ee mfalme, uishi milele. MUNGU WANGU AMEMTUMA MALAIKA WAKE, NAYE AMEYAFUMBA MAKANWA YA SIMBA, nao hawakunidhuru; kwa kuwa mbele zake mimi nalionekana kuwa sina hatia; tena, mbele yako, Ee mfalme, sikukosa neno. Basi mfalme akafurahi sana, akaamuru wamtoe Danieli katika lile tundu. Ndipo Danieli akatolewa katika lile tundu, wala dhara lo lote halikuonekana mwilini mwake, kwa sababu alikuwa anamtumaini Mungu wake. Mfalme akaamuru, nao wakawaleta wale watu waliomshitaki Danieli, wakawatupa katika tundu la simba, wao, na watoto wao, na wake zao; na wale simba wakawashinda wakaivunja mifupa yao vipande vipande, kabla hawajafika chini ya tundu.”

 

3.       Petro – Mwanafunzi mmoja aliyekuwa mwema sana nyakati za Kanisa la kwanza huko Yafa kwa matendo yake mazuri kwa wajane na yatima aliyeitwa Thabita au Dorkas aliugua na kufa na walipokuwa wamemuosha walimuweka katika chumba na kumuita Petro, Petro alipokuja moja ya njia aliyoitumia kumuombea marehemu ilikuwa ni kwa maombi ya kupiga magoti na kwa kweli kwa kutumuia maombi hayo yaliyojaa unyenyekevu mkubwa maiti (Drkas aliyekuwa amekufa)alifufuka

 

Matendo 9:36-42 “Na mwanafunzi mmoja alikuwako Yafa, jina lake Tabitha, tafsiri yake ni Dorkasi (yaani paa); mwanamke huyu alikuwa amejaa matendo mema na sadaka alizozitoa. Ikawa siku zile akaugua, akafa; hata walipokwisha kumwosha, wakamweka orofani. Na kwa kuwa mji wa Lida ulikuwa karibu na Yafa, nao wanafunzi wamesikia ya kwamba Petro yuko huko, wakatuma watu wawili kwake, kumsihi na kusema, Usikawie kuja kwetu.  Petro akaondoka akafuatana nao. Alipofika, wakampeleka juu orofani wajane wote wakasimama karibu naye, wakilia na kumwonyesha zile kanzu na nguo alizozishona Dorkasi wakati ule alipokuwa pamoja nao. Petro akawatoa nje wote, AKAPIGA MAGOTI, AKAOMBA, kisha akaelekea yule maiti, akanena, Tabitha, ondoka. Naye akafumbua macho yake, na alipomwona Petro akajiinua, akaketi. Akampa mkono, akamwinua; hata akiisha kuwaita wale watakatifu na wajane akamweka mbele yao, hali yu hai. Ikajulikana katika mji mzima wa Yafa; watu wengi wakamwamini Bwana.”

 

Ni kama tunajifunza hapo kuwa maombi ya kupiga magoti yanaweza kusababisha muujiza mkubwa sana na kuleta nguvu ya ajabu kwani sio tu mtu alifufuka lakini wengi pia waliosikia habari za tukio hilo katika mji huo na vitongoji vyake walimuamini Bwana kupitia muujiza ule, Unyenyekevu mkubwa kwa Mungu kwa njia ya kupiga magoti unaweza kufungua udhihirisho mkubwa sana wa nguvu za Mungu.

 

4.       Suleimani – alikuwa ni mfalme mwenye utukufu mkubwa na wa hali ya juu lakini hakuacha kuonyesha unyenyekevu kwa Mungu wake siku ya kuweka wakfu Hekalu alipiga magoti na kuomba maombi maalumu sana mbele ya watu wote bila kujali heshima yake na cheo chake jambo lililopeleka siku ile moto wa Mungu ukashuka na kuteketeza sadaka ya kutekeketezwa na utukufu wa Mungu ukashuka katika nyumba ya Mungu siku ile ilipokuwa inawekwa wakfu jambo lililosababisha makuhani kushindwa kutekeleza majukumu yao

 

2Nyakati 6:13-17. “(maana Sulemani alikuwa amefanya mimbari ya shaba, urefu wake mikono mitano, na upana wake mikono mitano, na kwenda juu kwake mikono mitatu, na kuisimamisha katikati ya ua; akasimama juu yake, AKAPIGA MAGOTI MBELE YA MKUTANO WOTE WA ISRAELI, AKAIKUNJUA MIKONO YAKE KUELEKEA MBINGUNI); akasema, Ee Bwana, Mungu wa Israeli, hakuna Mungu kama wewe, mbinguni, wala duniani; ushikaye maagano na rehema kwa watumishi wako, waendao mbele zako kwa moyo wao wote; uliyemtimizia mtumishi wako Daudi, baba yangu, ahadi uliyomwahidi; naam, ulinena kwa kinywa chako, ukayatimiza kwa mkono wako, kama ilivyo leo. Sasa, Ee Bwana, Mungu wa Israeli, umfikilizie mtumishi wako Daudi, baba yangu, ahadi uliyomwahidia, ukisema, Hutakosa kuwa na mtu machoni pangu, wa kuketi katika kiti cha enzi cha Israeli; wakiwa tu watoto wako wataiangalia njia yao, ili kuiendea torati yangu, kama wewe ulivyokwenda mbele zangu.Basi sasa, Ee Bwana, Mungu wa Israeli, ulithibitishe neno lako, ulilomwambia mtumishi wako Daudi.”

 

2Nyakati 7:1-4. “Basi Sulemani alipokwisha maombi hayo, moto ukashuka kutoka mbinguni, ukateketeza sadaka ya kuteketezwa na dhabihu; utukufu wa Bwana ukaijaza nyumba. Wala makuhani hawakuweza kuingia nyumbani mwa Bwana, kwa kuwa utukufu wa Bwana umeijaza nyumba ya Bwana. Wakatazama wana wa Israeli wote, uliposhuka ule moto, utukufu wa Bwana ulipokuwapo juu ya nyumba; wakasujudu kifulifuli hata nchi sakafuni, wakaabudu, wakamshukuru Bwana, wakisema, Kwa kuwa ni mwema; kwa maana fadhili zake ni za milele. Ndipo mfalme na watu wote wakatoa dhabihu mbele za Bwana.”

 

Ni kama tunajifunza hapo kuwa kumbe maombi ya unyenyekevu ya kumpigia Mungu magoti yanaweza kusababisha Mungu kushuka kwa utukufu na uwepo wake katika namna ambayo ni ya kipekee na ni nani asiyependa kuuona utukufu wa Bwana? Mungu alishuka na Mungu anaweza kushuka kwa kumpigia magoti

 

Stephano – Alikuwa anazingirwa na maadui na walikuwa wamekusudia kumuua baada ya kushindwa kwa hoja kutokana na ukinzani wa kidini, walimkasirikia sana Stephano, walimsagia meno na wakiwa wamekusudia kutaka kumuua na akiwa katika mateso na kukabiliwa na hali ya kifo alipiga magoti, aliwasamehe adui zake alimuona Yesu amesiamama tayari kumpokea na walipomkazia macho waliona uso wake ni kama wa malaika haya yanamtokea mtu huyu wa Mungu wa kipekee akiwa amepiga magoti na kumuomba Mungu

 

Matendo 6:8-15 “Na Stefano, akijaa neema na uwezo, alikuwa akifanya maajabu na ishara kubwa katika watu. Lakini baadhi ya watu wa sinagogi lililoitwa sinagogi la Mahuru, na la Wakirene, na la Waiskanderia, na la wale wa Kilikia na Asia, wakaondoka na kujadiliana na Stefano; lakini hawakuweza kushindana na hiyo hekima na huyo Roho aliyesema naye. Hata wakashawishi watu waliosema, Tumemsikia mtu huyu akinena maneno ya kumtukana Musa na Mungu. Wakawataharakisha watu na wazee na waandishi, wakamwendea, wakamkamata, wakampeleka mbele ya baraza. Wakasimamisha mashahidi wa uongo waliosema, Mtu huyu haachi kusema maneno ya kufuru juu ya mahali hapa patakatifu na juu ya torati; maana tumemsikia akisema kwamba Yesu huyo Mnazareti atapaharibu mahali hapa, na kuzibadili desturi tulizopewa na Musa. Watu wote walioketi katika ile baraza wakamkazia macho yao, wakamwona uso wake kuwa kama uso wa malaika.”

 

Matendo 7:57-60 “Wakapiga kelele kwa sauti kuu, wakaziba masikio yao, wakamrukia kwa nia moja, wakamtoa nje ya mji, wakampiga kwa mawe. Nao mashahidi wakaweka nguo zao miguuni pa kijana mmoja aliyeitwa Sauli. Wakampiga kwa mawe Stefano, naye akiomba, akisema, Bwana Yesu, pokea roho yangu. AKAPIGA MAGOTI, AKALIA KWA SAUTI KUU, BWANA, USIWAHESABIE DHAMBI HII. Akiisha kusema haya akalala. Na Sauli alikuwa akiona vema kwa kuuawa kwake.”

 

Paulo – Akiwa katika mafundisho na mkazo wa kiroho kwa wazee na washirika wa kanisa la Efeso wakati anakamilisha huduma yake huko hatimaye Paulo na wote waliokuwa wakimsindikiza walipiga magoti na kumuomba Mungu Neema kwa pamoja

 

Matendo 20:31-38 “Kwa hiyo kesheni, mkikumbuka ya kwamba miaka mitatu, usiku na mchana, sikuacha kumwonya kila mtu kwa machozi. Basi, sasa nawaweka katika mikono ya Mungu, na kwa neno la neema yake, ambalo laweza kuwajenga na kuwapa urithi pamoja nao wote waliotakaswa. Sikutamani fedha wala dhahabu, wala mavazi ya mtu. Ninyi wenyewe mnajua ya kuwa mikono yangu hii imetumika kwa mahitaji yangu na ya wale waliokuwa pamoja nami. Katika mambo yote nimewaonyesha ya kuwa kwa kushika kazi hivi imewapasa kuwasaidia wanyonge, na kuyakumbuka maneno ya Bwana Yesu, jinsi alivyosema mwenyewe, Ni heri kutoa kuliko kupokea. ALIPOKWISHA KUNENA HAYA AKAPIGA MAGOTI, AKAOMBA PAMOJA NAO WOTE. Wakalia sana wote, wakamwangukia Paulo shingoni, wakambusu-busu, wakihuzunika zaidi kwa sababu ya neno lile alilosema, ya kwamba hawatamwona uso tena. Wakamsindikiza hata merikebuni.”

 

Tunajifunza hapa kuwa kupiga magoti pia inaweza kuwa ni hali ya kawaida ya maisha ya kila siku ya kumuomba Mungu kwa wakristo na viongozi wa kanisa, sio tu wakati wa changamoto lakini kwaajili ya kijiumbia tabia ya unyenyekevu tunaweza kuitumia njia hii kila wakati na Mungu akajali na kusikiliza dua zetu.

Yakobo Ndugu yake Bwana – Kwa mujibu wa masimulizi ya tamaduni za nyakati za kanisa la Kwanza inaelezewa kuwa Yakobo Ndugu yake Bwana alikuwa ni moja ya watu waliokuwa waombaji hodari sana kwa kupiga magoti, kiasi ambacho alipewa jina la Mtu mwenye magoti ya ngamia,  kwa mujibu wa maelezo ya mwanahistoria wa kanisa wa karne ya pili aliyeitwa Eusebius alinukuu maelezo ya Hegesippus yakieleza kuwa Yakobo ndugu yake Yesu alikuwa na tabia ya kupiga magoti hekaluni na kuomba kwa muda mrefu kiasi ambacho magoti yake yalishika sugu kama magoti ya ngamia, aliheshimiwa sana kwa sababu alisikika akiwaombea watu na kutubia dhambi zao, kwa kupiga magoti pembezoni mwa hekalu hii ilikuwa ni desturi yake ya maisha mpaka alipouawa kwa kupigwa mawe ambapo pia alipiga magoti na kuomba Baba uwasamehe, tunajifunza kwake kuwa kanisa pamoja na maombi mengine wakati mwingine ni vema kuwa na muda wa unyenyekevu na kukaa magotini kwa muda wa kutosha ili tuweze kupata rehema kwa Mungu wetu

Nguvu ya kuomba kwa kupiga magoti.

Kupiga magoti kama kutaanza kutokea ndani yaani moyoni ni moja ya silaha yenye nguvu sana katika maombi, sisemi kwamba kila anayepiga magoti maombi yake yanaweza kujibiwa, wala sisemi kuwa maombi ya kupiga magoti ni muhimu kuliko ya iana nyingine  lakini  nasema kile maandiko yamekionyesha swala Muhimu hapa ni kuvunjika moyo, ni kunyenyekea, ni kupondeka mbele za Mungu ishara yake ya nje ndio kupiga magoti, Kuna nguvu ya kusikilizwa na Mungu mtu anapokwenda mbele za Mungu au wakili wa Mungu kwa kuvunjika au kwa unyenyekevu ni  kama kunahusisha toba, unyenyekevu ibada na kuvunjiia vunjika mbele za Mungu, ni tendo ambalo likifanyika kuanzia moyoni linakupatia kibali na linaongezea neema hii ni kwa sababu Mungu huangalia moyo, kwa kupiga magoti kutoka moyoni unajitengenezea kibali kwa Mungu na kumfanya Mungu akuhurumie kwa haraka hitaji lako:-

2Wafalme 1:9-14 “Ndipo mfalme akatuma akida wa askari hamsini pamoja na hamsini wake, wamwendee Eliya. Akamwendea, na tazama, ameketi juu ya kilima. Akamwambia, Ewe mtu wa Mungu, mfalme asema, Shuka. Eliya akajibu, akamwambia yule akida wa hamsini, Ikiwa mimi ni mtu wa Mungu, na ushuke moto kutoka mbinguni, ukuteketeze wewe na hamsini wako. Moto ukashuka, ukamteketeza, yeye na hamsini wake. Akatuma tena akida wa hamsini mwingine pamoja na hamsini wake, wamwendee. Akajibu, akamwambia, Ewe mtu wa Mungu, mfalme asema, Shuka upesi. Eliya akajibu, akamwambia, Ikiwa mimi ni mtu wa Mungu, na ushuke moto kutoka mbinguni, ukuteketeze wewe na hamsini wako. Moto wa Mungu ukashuka kutoka mbinguni, ukamteketeza, yeye na hamsini wake. Tena akatuma akida wa hamsini wa tatu, pamoja na hamsini wake. Yule akida wa hamsini wa tatu akapanda, AKAENDA AKAPIGA MAGOTI mbele ya Eliya, akamsihi sana, akamwambia, Ee mtu wa Mungu, nakusihi, roho yangu, na roho za watumishi wako hawa hamsini, ziwe na thamani machoni pako. Tazama, moto ulishuka kutoka mbinguni, ukawateketeza wale akida wa hamsini wawili wa kwanza pamoja na hamsini wao; laiti sasa roho yangu na iwe na thamani machoni pako. Malaika wa Bwana akamwambia Eliya, Shuka pamoja naye; usimwogope. Akaondoka, akashuka pamoja naye hata kwa mfalme.”

Akida hawa wa askari wa kikosi chenye askari 50 wa kwanza na wa pili  waliuawa kwa sababu ya tabia na mwenendo wao wa kutokujali mamlaka ya kiungu, walimuamuru Nabii ashuke na kumtii mfalme lakini nabii alikuwa anawakilisha mamlaka ya Mungu, na Mungu aliangalia kutoka moyoni  na kuwaona maakida hao kuwa kwa maneno na vitendo walikuwa hawana adabu,  wala moyo wa unyenyekevu, moyo wa akida wa 3 wa kikosi cha 50 mwengine yeye alikuwa na unyenyekevu wa hali ya juu sana na kwa sababu hiyo alipata neema kwa hiyo tabia ya kiburi kutoka moyoni inaweza kusababisha dua yako au yangu isisikilizwe na tabia ya unyenyekevu na kuvunjika kutoka moyoni huvutia neema ya Mungu, kwa hiyo kupiga magoti ni lazima kuwe kumetoka moyoni mtu anaweza kupiga magoti kwa nje lakini kwa nia na lengo la kudhihaki kama askari waliomsulubisha Yesu walivyomfanyia, walipiga magoti kwa dhihaka na sio kwaajili ya kunyenyekea bali kudhalilisha, hii ilikuwa ni jeuri ya wazi ya mwanadamu dhidi ya mwana wa Mungu ambaye kila goti litapigwa kwake

Mathayo 27:27-31 “Ndipo askari wa liwali wakamchukua Yesu ndani ya Praitorio, wakamkusanyikia kikosi kizima.Wakamvua nguo, wakamvika vazi jekundu. Wakasokota taji ya miiba, wakaiweka juu ya kichwa chake, na mwanzi katika mkono wake wa kuume; WAKAPIGA MAGOTI MBELE YAKE, WAKAMDHIHAKI, wakisema, Salamu, Mfalme wa Wayahudi! Kisha wakamtemea mate, wakautwaa ule mwanzi, wakampiga-piga kichwani. Walipokwisha kumdhihaki, wakalivua lile vazi, wakamvika mavazi yake, wakamchukua kumsulibisha.”

Mtu mwenye ukoma aliyechoshwa na hali ya kukaa na ukoma alimjia Yesu na kumpigia magoti akihitaji rehema za Mungu na kwa huruma kubwa sana, Yesu alimkubalia ombi lake kwa huruma na akatakakaswa ukoma kwa mamlaka

Marko 1:40-42 “Akaja kwake mtu mwenye ukoma, akamsihi na kumpigia magoti, na kumwambia, Ukitaka, waweza kunitakasa. Naye akamhurumia, akanyosha mkono wake, akamgusa, akamwambia, Nataka, takasika. Na mara ukoma wake ukamtoka, akatakasika.”

Uko umuhimu wa kumuendea Mungu kwa heshima na unyenyekevu mkubwa, sisi hatuwezi lolote kwake yeye ni Muumba na sisis ni viumbe, kuokolewa kwetu kusitufanye sisi kujifikiri kuwa ni wa Muhimu sana na hata kama tutajifikiri kuwa ni wa Muhimu kwa Mungu wetu bado inatupasa kutambua kuwa yeye ni Bwana wa Mabwana na kuwa tukimuheshimu naye atatuheshimu, kupiga magoti ni ishara ya heshima kwa Mungu wetu naye anastahili, wote waliokwenda Mbele zake kwa unyenyekevu Mungu hakuwahi kuwaangusha na hii ndio nguvu ya kumuendea tukiwa tumepiga magoti mbele zake  kama ishara kutoka moyoni kuwa tunavunjika mbele zake, tu wanyonge mbele zake hebu kuanzia sasa jaribu kujifunza namna na jinsi tunavyopaswa kukaa magotini kwake

1Samuel 2:30 “Kwa sababu hiyo, Bwana, Mungu wa Israeli, asema, Ni kweli, nalisema ya kuwa nyumba yako, na nyumba ya baba yako itakwenda mbele zangu milele; lakini sasa Bwana asema, Jambo hili na liwe mbali nami; kwa maana wao wanaoniheshimu nitawaheshimu, na wao wanaonidharau watahesabiwa kuwa si kitu.”

Isaya 66:2 “Maana mkono wangu ndio uliofanya hivi vyote, vitu hivi vyote vikapata kutokea, asema Bwana; lakini mtu huyu ndiye nitakayemwangalia, mtu aliye mnyonge, mwenye roho iliyopondeka, atetemekaye asikiapo neno langu.”

Na. Rev. Innocent Samuel Kamote

Mkuu wa wajenzi mwenye Hekima 

Jumatatu, 25 Mei 2026

Yawafaa ninyi Mimi niondoke!

 


Yohana 16:7-13 “Lakini mimi nawaambia iliyo kweli; yawafaa ninyi mimi niondoke, kwa maana mimi nisipoondoka, huyo Msaidizi hatakuja kwenu; bali mimi nikienda zangu, nitampeleka kwenu. Naye akiisha kuja, huyo atauhakikisha ulimwengu kwa habari ya dhambi, na haki, na hukumu. Kwa habari ya dhambi, kwa sababu hawaniamini mimi; kwa habari ya haki, kwa sababu mimi naenda zangu kwa Baba, wala hamnioni tena; kwa habari ya hukumu, kwa sababu yule mkuu wa ulimwengu huu amekwisha kuhukumiwa. Hata bado nikali ninayo mengi ya kuwaambia, lakini hamwezi kuyastahimili hivi sasa. Lakini yeye atakapokuja, huyo Roho wa kweli, atawaongoza awatie kwenye kweli yote; kwa maana hatanena kwa shauri lake mwenyewe, lakini yote atakayoyasikia atayanena, na mambo yajayo atawapasha habari yake.”



Utangulizi:

Ni muhimu kufahamu kuwa Yesu Kristo alikuwa anazungumza maneno haya mwishoni kabisa mwa huduma yake akiwa amewaaga wanafunzi wake ya kuwa yeye ameikamilisha kazi aliyotumwa kuifanya na kuwa anarudi kwa Baba, Yesu alikuwa amewaeleza wanafunzi wake kuwa atasulubiwa, kufa na kufufuka, na kuikamilisha kazi ya ukombozi wa mwanadamu, na baada yake nini kingelifuata. Yesu anaonyesha kwa uwazi umuhimu wa kuja kwa Roho Mtakatifu, hili lilikuwa ni jambo la muhimu sana kwani lingeondoa hofu ya wanafunzi wake na kuifanya kazi ya Mungu kupanuka kwa kina zaidi na hivyo kuondoka kwake kulikuwa na faida zaidi kuliko hasara ambayo wanafunzi wake walikuwa wakiifikiria, Yesu alikuwa anafahamu changamoto ambazo zingewakabili wanafunzi wake baada yake na hivyo alitaka kuwathibitishia kuwa uwepo wa Roho Mtakatifu utakuwa na umuhimu zaidi na suluhu kwa hofu yao

Yohana 14:16-17 “Nami nitamwomba Baba, naye atawapa Msaidizi mwingine, ili akae nanyi hata milele; ndiye Roho wa kweli; ambaye ulimwengu hauwezi kumpokea, kwa kuwa haumwoni wala haumtambui; bali ninyi mnamtambua, maana anakaa kwenu, naye atakuwa ndani yenu.”

Kimsingi Yesu Kristo alilizungumzia swala na ujio wa Roho Mtakatifu kama swala muhimu sana  na hitaji la msingi katika maisha ya kiroho ya  wanafunzi wake na kila aaminiye  baadaye na huduma, Yesu alitaka wanafunzi wake wawe na uelewa mpana kuhusu umuhimu wa Roho Mtakatifu na kuonyesha wazi kuwa hatuwezi kwa namna yoyote ile kuishi duniani na kutimiza kusudi la Mungu bila msaada wa Roho Mtakatifu na nguvu zake mwenyewe, kwa msingi huo katika msimu huu wa juma la Pentekoste tutachukua  muda kutafakari kwa kina na mapana  na marefu umuhimu wa Roho Mtakatifu katika maisha yetu, na kujumuika kwa pamoja katika maombezi ya ubatizo wa Roho Mtakatifu na  hivyo tutajifunza somo hili “Yawafaa ninyi mimi niondoke” kwa kuzingatia vipengele vitatu vifuatavyo:

·         Yawafaa ninyi mimi niondoke

·         Kazi za Roho Mtakatifu Duniani

·         Ubatizo wa Roho Mtakatifu

Yawafaa ninyi mimi niondoke!

Kimsingi Roho Mtakatifu ametolewa na Mungu Baba yetu ili akae nasi milele na kuikamilisha ile kazi iliyoanzishwa na Yesu Kristo hapa duniani, Yesu alikuwa hana budi kuteswa na kufa msalabani kisha kufufuka siku ya tatu na kupaa kwenda mbinguni mpaka wakati ulioamriwa, Ujio wa Roho Mtakatifu ulikuwa ni wa Muhimu sana kwa sababu kuweko wa Yesu Duniani katika mwili wa kibinadamu kulimpa mipaka ya kihuduma na alilazimika kuweko mahali pamoja kwa wakati mmoja lakini kwa kitendo cha kupaa na kurudi kwa Baba angetoa ruhusa kwa Roho Mtakatifu kuja na kukaa na sisi daima  na kuuleta uwepo wa Mungu kwa kila mmoja kokote aliko Duniani, Kutokana na umuhimu wa Roho Mtakatifu, Yesu aliwaagiza wanafunzi wake kutokuianza kazi ya Mungu kwanza mpaka wamepokea ubatizo wa Roho Mtakatifu ambaye angewageuza,  kuwapa nguvu na kuwafanya kuwa mashahidi wake

Matendo 1:4-8 “Hata alipokuwa amekutana nao aliwaagiza wasitoke Yerusalemu, bali waingoje ahadi ya Baba, ambayo mlisikia habari zake kwangu; ya kwamba Yohana alibatiza kwa maji, bali ninyi mtabatizwa katika Roho Mtakatifu baada ya siku hizi chache. Basi walipokutanika, wakamwuliza, wakisema, Je! Bwana, wakati huu ndipo unapowarudishia Israeli ufalme? Akawaambia, Si kazi yenu kujua nyakati wala majira, Baba aliyoyaweka katika mamlaka yake mwenyewe. Lakini mtapokea nguvu, akiisha kuwajilia juu yenu Roho Mtakatifu; nanyi mtakuwa mashahidi wangu katika Yerusalemu, na katika Uyahudi wote, na Samaria, na hata mwisho wa nchi.”

Luka 24:46-49 “Akawaambia, Ndivyo ilivyoandikwa, kwamba Kristo atateswa na kufufuka siku ya tatu; na kwamba mataifa yote watahubiriwa kwa jina lake habari ya toba na ondoleo la dhambi, kuanza tangu Yerusalemu. Nanyi ndinyi mashahidi wa mambo haya. Na tazama, nawaletea juu yenu ahadi ya Baba yangu; lakini kaeni humu mjini, hata mvikwe uwezo utokao juu.”

Wanafunzi wa Yesu Kristo walikuwa pamoja naye kwa zaidi ya miaka mitatu na nusu, wakijifunza maarifa elimu na uwezo wa kufanya huduma lakini pamoja na yote haya Yesu anawaamuru wasitoke kufanya lolote mpaka wapokee ahadi ya Baba, hii ilikuwa na maana iliyo wazi ya kuwa Elimu, ujuzi na maarifa pekee hautoshi, uzoefu hautoshi, vipawa vya kibinadamu havitoshi ili tuwe wanafunzi wa Yesu waliokamilika tunamuhitaji sana Roho Mtakatifu. Uwepo wa Roho Mtakatifu ambaye haonekani kwa macho katika maisha ya wanafunzi wa Yesu ni wa muhimu zaidi kuliko uwepo wa Yesu katika hali ya mwili, Roho Mtakatifu asingeliweza kuja kama Yesu angeendelea kubaki, Kupaa kwa Yesu Kristo, na kutukuzwa kwake mbinguni kungeruhusu ujio wa Roho Mtakatifu ambaye uwepo wake ungesababisha uwepo wa Mungu kukaa ndani ya kila mwamini kokote aliko duniani, lakini pia kazi ya kutukuzwa kwa Yesu Kristo Duniani  ingeanza kupitia Roho Mtakatifu sawasawa na jinsi ambavyo Yesu ametukuzwa Mbinguni.

Kazi za Roho Mtakatifu Duniani

-          Roho Mtakatifu ni Msaidizi mwingine – Yesu Kristo alikuwa anafahamu kuwa Wanafunzi wake wangekabiliwa na changamoto kali  na kubwa na upinzani mkali wa aina mbalimbali na wangekata tamaa hasa baada ya kuondoka kwake, Yeye alipokuwa pamoja nao alikuwa ni mtetezi mkubwa sana wa wanafunzi wake na mashambulizi yote ya adui yalielekezwa kwake, Kuondoka kwake Yesu Kristo ilikuwa sababu ya huzuni nyingi sana hofu na mashaka na walikata tamaa, Yesu aliwaahidi kuwa atawaletea msaidizi mwingine

 

Yohana 14:16-17 “Nami nitamwomba Baba, naye atawapa Msaidizi mwingine, ili akae nanyi hata milele; ndiye Roho wa kweli; ambaye ulimwengu hauwezi kumpokea, kwa kuwa haumwoni wala haumtambui; bali ninyi mnamtambua, maana anakaa kwenu, naye atakuwa ndani yenu.”

 

Neno Msaidizi mwingine katika lugha ya kiyunani (Koine Greek) linasomeka kama “Paraklētos” ambalo maana yake Msaidizi, mtetezi, mfariji, mshauri au mtu anayesimama karibu na wewe kwa kusudi la kukutetea wakili (Advocate) Kazi hii inafanywa na Roho Mtakatifu kwa kila mtu aliyemuamini hata leo, kwa sababu hiyo kila mtu aliyeokoka anamuhitaji yeye kama uwepo wa Mungu katika maisha yetu ya kila siku.

 

-          Roho Mtakatifu anauwezo wa kubadilisha maisha – Wanafunzi wa Yesu Kristo walikuwa wanahitaji mabadiliko makubwa ya maisha yao, wengine walikuwa waoga, wasiojiamini, wenye ukali, wenye kisasi, wasioweza kusamehe na walihitaji mabadiliko makubwa sana, Roho Mtakatifu ndiye njia inayohusika katika mfumo mzima wa kubadili maisha ya mtu na kumfanya afae kwa kazi ile ambayo Mungu anaihiitahi katika maisha, ni pale tu Roho wa Mungu anapokuwa juu ya mtu kwa ubatizo ndipo anapoweza kubadilisha maisha ya mtu huyo na kumfanya afae kwa matumizi ya kazi ya ufalme wa Mungu.

 

1Samuel 10:5-7 “Baada ya hayo utafika Gibea ya Mungu, hapo palipo na ngome ya Wafilisti; kisha itakuwa, utakapofika mjini, utakutana na kundi la manabii wakishuka kutoka mahali pa juu, wenye kinanda, na tari, na kinubi, na filimbi mbele yao, nao watakuwa wakitabiri; na roho ya Bwana itakujilia kwa nguvu, nawe utatabiri pamoja nao, nawe utageuzwa kuwa mtu mwingine. Basi, hapo ishara hizi zitakapokutukia, fanya kama uonavyo vema; kwa kuwa Mungu yu pamoja nawe.”

 

Wagalatia 5:16-25 “Basi nasema, Enendeni kwa Roho, wala hamtazitimiza kamwe tamaa za mwili. Kwa sababu mwili hutamani ukishindana na Roho, na Roho kushindana na mwili; kwa maana hizi zimepingana, hata hamwezi kufanya mnayotaka. Lakini mkiongozwa na Roho, hampo chini ya sheria. Basi matendo ya mwili ni dhahiri, ndiyo haya, uasherati, uchafu, ufisadi, ibada ya sanamu, uchawi, uadui, ugomvi, wivu, hasira, fitina, faraka, uzushi,husuda, ulevi, ulafi, na mambo yanayofanana na hayo, katika hayo nawaambia mapema, kama nilivyokwisha kuwaambia, ya kwamba watu watendao mambo ya jinsi hiyo hawataurithi ufalme wa Mungu.Lakini tunda la Roho ni upendo, furaha, amani, uvumilivu, utu wema, fadhili, uaminifu, upole, kiasi; juu ya mambo kama hayo hakuna sheria. Na hao walio wa Kristo Yesu wameusulibisha mwili pamoja na mawazo yake mabaya na tamaa zake.Tukiishi kwa Roho, na tuenende kwa Roho.”

 

Ubatizo wa Roho Mtakatifu unatubadilisha maisha na kutufanya au kutusaidia kuishi maisha matakatifu siku hadi siku, kutembea katika Roho Mtakatifu kutayafanya maisha yetu yaachane na zile hali za mwili na kuruhusu ukomavu na kuzaliwa kwa matunda ya Roho Mtakatifu katika maisha yetu na kumlingania Yesu.

 

-          Roho Mtakatifu hutuvika uwezo au Nguvu kutoka juu – Kuihubiri injili na kuishi maisha ya ushuhuda kunahitaji nguvu za Mungu, Mungu anapowatuma watu katika ulimwengu huu anawavika nguvu kwa sababu kuna nguvu za upinzani ambazo tutakabiliana nazo duniani nguvu hii  tunayovikwa na Roho wa Mungu katika lugha ya kitaalamu ya maandiko ya agano jipya inaitwa “Dunamis” hili ni neno la Kiyunani (Koine Greek) ambalo lina maanisha uwezo, nguvu za Mungu, Nguvu zenye matokeo na mamlaka, nguvu hii husaidia waamini kukabiliana na upinzani wa anaina yoyote na kuwa tayari hata kufa kwaajili ya jina la Bwana na kwaajili ya ufalme wa Mungu, Wale waliokuwa na hofu na woga waliweza kutiwa nguvu na kuwa majasiri mara baada ya kubatizwa katika Roho Mtakatifu, tutakuwa na uwezo wa kukabiliana na upinzani wa aina yoyote na kuwa tayari hata kufa kwaajili ya jina la Bwana kama tutabatizwa kwa Roho Mtakatifu.

 

Luka 24:46-49 “Akawaambia, Ndivyo ilivyoandikwa, kwamba Kristo atateswa na kufufuka siku ya tatu; na kwamba mataifa yote watahubiriwa kwa jina lake habari ya toba na ondoleo la dhambi, kuanza tangu Yerusalemu. Nanyi ndinyi mashahidi wa mambo haya. Na tazama, nawaletea juu yenu ahadi ya Baba yangu; lakini kaeni humu mjini, hata mvikwe uwezo utokao juu.”

 

Matendo 1:8 “Lakini mtapokea nguvu, akiisha kuwajilia juu yenu Roho Mtakatifu; nanyi mtakuwa mashahidi wangu katika Yerusalemu, na katika Uyahudi wote, na Samaria, na hata mwisho wa nchi.”

 

-          Roho Mtakatifu atatuongoza katika kweli yote – Kweli yote ya Mungu haiwezi kueleweka kwa akili za kawaida peke yake, Lakini Roho Mtakatifu ni Mwalimu, yeye ni mwandishi wa neno la Mungu, ni Mwalimu na anaweza kutupa ufunuo wa kweli,  lakini sio hivyo tu Roho Mtakatifu atatukumbusha katika maswala yote muhimu na ya msingi katika mafundisho ya Yesu Kristo, Yeye hufanya kazi ya kutufunulia maswala yote kuhusu Mungu na mapenzi yake, Katika ulimwengu huu kila mtu anadai anayo kweli lakini ni kazi ya Roho Mtakatifu ambaye anaitwa Roho wa kweli kuufunua ukweli halisi sawasawa na ufunuo wa neno la Mungu.

 

Yohana 14:26 “  Lakini huyo Msaidizi, huyo Roho Mtakatifu, ambaye Baba atampeleka kwa jina langu, atawafundisha yote, na kuwakumbusha yote niliyowaambia.”

 

1Wakorintho 2:10-14 “Lakini Mungu ametufunulia sisi kwa Roho. Maana Roho Huchunguza yote, hata mafumbo ya Mungu, Maana Ni nani katika binadamu ayajuaye mambo ya binadamu ila roho ya binadamu iliyo ndani yake? Vivyo hivyo na mambo ya Mungu hakuna ayafahamuye ila Roho wa Mungu. Lakini sisi hatukuipokea roho ya dunia, bali Roho atokaye kwa Mungu, makusudi tupate kuyajua tuliyokirimiwa na Mungu.  Nayo twayanena, si kwa maneno yanayofundishwa kwa hekima ya kibinadamu, bali yanayofundishwa na Roho, tukiyafasiri mambo ya rohoni kwa maneno ya rohoni. Basi mwanadamu wa tabia ya asili hayapokei mambo ya Roho wa Mungu; maana kwake huyo ni upuzi, wala hawezi kuyafahamu, kwa kuwa yatambulikana kwa jinsi ya rohoni.”

 

-          Roho Mtakatifu humshuhudia Yesu Kristo – Kumshuhudia Yesu Kristo katika lugha ya asili ya kiyunani linatumika neno “martureō ambalo kwa kiingereza ni sawa na  neno “giving evidence”, au “well report about me”, maana yake ni kuwa Roho Mtakatifu atathibitisha ukweli kuhusu Yesu Kristo ni nani au ataelezea vizuri kuhusu Yesu Kristo, ana ushahidi wa kina kuhusu Yesu Kristo, kwa hiyo kama Mwalimu wa kweli atawaelekeza watu kumjua Yesu Kristo kwa kina zaidi ya alivyojulikana kwa wakati ule, na anavyoelezewa katika maandiko, atamuinua Yesu Kristo atathibitisha mafundisho yake kwa hiyo huduma yoyote ya kiroho au inayoongozwa kiroho haitakuwa na malengo ya kumuinua mtu bali itakuwa inamuinua Yesu Kristo, huduma yoyote ambayo haimuinui Yesu Kristo inahitaji kupimwa , na mtumishi yoyote ambaye hamuinui Yesu hatuna budi kumwangalia kwa makini na nabii yeyote ambaye anajitukuza yeye kuliko Kristo naye ni wa kuangaliwa kwa makini, ukiona imani yoyote inamuinua yeyote zaidi ya Kristo basi ni imani yenye mashaka.

 

Yohana 15:26 “Lakini ajapo huyo Msaidizi, nitakayewapelekea kutoka kwa Baba, huyo Roho wa kweli atokaye kwa Baba, yeye atanishuhudia.”

 

1Wakorintho 12:3Kwa hiyo nawaarifu, ya kwamba hakuna mtu anenaye katika Roho wa Mungu, kusema, Yesu amelaaniwa; wala hawezi mtu kusema, Yesu ni Bwana, isipokuwa katika Roho Mtakatifu.”

-          Roho Mtakatifu hutoa nyenzo za kutendea kazi – Ziko nyenzo za kutendea kazi ya Mungu ambazo hutolewa na Roho Mtakatifu ni maarufu sana kama karama za Roho Mtakatifu, hizi husaidia kurahisisha kazi ya Mungu na kulithibitisha neno na kuufaidia mwili wa Kristo, bila karama na utendaji wa Roho Mtakatifu kupitia karama hizo maneno yetu yatakuwa ni maneno yasiyo na uthibitisho au yanaweza kuwa kama hekima tu za wanadamu (Yaani Falsafa) au maneno ya kushawishi, lakini litakuwa ni neno lenye kuthibitishwa

 

1Wakorintho 2:4-5 “Na neno langu na kuhubiri kwangu hakukuwa kwa maneno ya hekima yenye kushawishi akili za watu, bali kwa dalili za Roho na za nguvu, ili imani yenu isiwe katika hekima ya wanadamu, bali katika nguvu za Mungu.”

 

1Wakorintho 12:7-11 “Lakini kila mmoja hupewa ufunuo wa Roho kwa kufaidiana. Maana mtu mmoja kwa Roho apewa neno la hekima; na mwingine neno la maarifa, apendavyo Roho yeye yule; mwingine imani katika Roho yeye yule; na mwingine karama za kuponya katika Roho yule mmoja; na mwingine matendo ya miujiza; na mwingine unabii; na mwingine kupambanua roho; mwingine aina za lugha; na mwingine tafsiri za lugha; lakini kazi hizi zote huzitenda Roho huyo mmoja, yeye yule, akimgawia kila mtu peke yake kama apendavyo yeye.”

 

-          Roho Mtakatifu ni njia ya kurahisisha ukomavu wa kiroho – Roho Mtakatifu anahusika katika kuzaliwa kwetu mara ya pili, lakini pia anahusika katika kusaidia ukomavu wetu wa kiroho, endapo Mkristo atakomaa kiroho matendo yote ya mwili yanapukutika na matunda ya kiroho yanaanza kujichomoza katika maisha ya mwamini, Roho Mtakatifu hatoi karama tu bali anatoa na matunda ambayo kimsingi hutuumbia tabia kama ya Kristo

 

Wagalatia 5:22-25 “Lakini tunda la Roho ni upendo, furaha, amani, uvumilivu, utu wema, fadhili, uaminifu, upole, kiasi; juu ya mambo kama hayo hakuna sheria. Na hao walio wa Kristo Yesu wameusulibisha mwili pamoja na mawazo yake mabaya na tamaa zake. Tukiishi kwa Roho, na tuenende kwa Roho.”

 

-          Roho Mtakatifu hutupa hekima ya utawala na maamuzi – Ili dunia iweze kuongozwa vema na maamuzi yaweze kufanyika kwa haki bila upendeleo wala kuumiza watu tunamuhitaji Roho Mtakatifu ambapo yeye hutoa hofu ya Mungu, haki, ufahamu, ushauri, uweza na maarifa yatakayosaidia kuujenga ufalme wa Mungu na kuiongoza dunia katika haki.

 

Isaya 11:1-5 “Basi litatoka chipukizi katika shina la Yese, na tawi litakalotoka katika mizizi yake litazaa matunda. Na roho ya Bwana atakaa juu yake, roho ya hekima na ufahamu, roho ya shauri na uweza, roho ya maarifa na ya kumcha Bwana; na furaha yake itakuwa katika kumcha Bwana; wala hatahukumu kwa kuyafuata ayaonayo kwa macho yake, wala hataonya kwa kuyafuata ayasikiayo kwa masikio yake; bali kwa haki atawahukumu maskini, naye atawaonya wanyenyekevu wa dunia kwa adili; naye ataipiga dunia kwa fimbo ya kinywa chake, na kwa pumzi ya midomo yake atawaua wabaya. Na haki itakuwa mshipi wa viuno vyake, na uaminifu mshipi wa kujifungia.”

 

Matendo 6:3-4 “Basi ndugu, chagueni watu saba miongoni mwenu, walioshuhudiwa kuwa wema, wenye kujawa na Roho, na hekima, ili tuwaweke juu ya jambo hili; na sisi tutadumu katika kuomba na kulihudumia lile Neno.”

 

-          Roho Mtakatifu hutupa nguvu za kukabiliana na uchawi – Katika ulimwengu huu tulio nao ziko nguvu kubwa mbili zinazotawala, nguvu za Mungu na nguvu za Giza, ili mwanadamu wa kawaida aweze kuwa na nguvu za Mungu zinazoweza kukabiliana na nguvu za giza ni lazima abatizwe katika Roho Mtakatifu, nguvu za Mungu kwetu ziko pia kwaajili ya kukabiliaana na nguvu pinzani  mfano

 

Matendo 13:6-12 “Walipokwisha kupita katikati ya kisiwa chote mpaka Pafo, wakaona mtu mmoja, mchawi, nabii wa uongo, Myahudi jina lake Bar-Yesu; mtu huyu alikuwa pamoja na liwali Sergio Paulo, mtu mwenye akili. Yeye liwali akawaita Barnaba na Sauli waje kwake, akataka kulisikia neno la Mungu. Lakini Elima, yule mchawi (maana ndiyo tafsiri ya jina lake), akashindana nao, akitaka kumtia yule liwali moyo wa kuiacha ile imani. Lakini Sauli, ambaye ndiye Paulo, akijaa Roho Mtakatifu, akamkazia macho, akasema, Ewe mwenye kujaa hila na uovu wote, mwana wa Ibilisi, adui wa haki yote, huachi kuzipotoa njia za Bwana zilizonyoka? Basi, angalia, mkono wa Bwana u juu yako, nawe utakuwa kipofu, usilione jua kwa muda. Mara kiwi kikamwangukia na giza, akazunguka-zunguka na kumtafuta mtu wa kumshika mkono na kumwongoza.Ndipo yule liwali, alipoyaona yaliyotendeka, akaamini, akiyastaajabia mafundisho ya Bwana.”

 

2Timotheo 3:8 “Na kama vile Yane na Yambre walivyopingana na Musa, vivyo hivyo na hawa wanapingana na ile kweli; ni watu walioharibika akili zao, wamekataliwa kwa mambo ya imani.”

 

1Wafalme 18 :21-24 “Naye Eliya akawakaribia watu wote, akanena, Mtasita-sita katikati ya mawazo mawili hata lini? Bwana akiwa ndiye Mungu, mfuateni; bali ikiwa Baali ni Mungu, haya! Mfuateni yeye. Wale watu hawakumjibu neno. Ndipo Eliya akawaambia watu, Mimi nimesalia, mimi peke yangu, nabii wa Bwana; lakini manabii wa Baali ni watu mia nne na hamsini. Kwa hiyo na watutolee ng'ombe wawili; wao na wajichagulie ng'ombe mmoja, wamkate-kate na kumweka juu ya kuni, wasitie moto chini; nami nitamtengeza huyo ng'ombe wa pili, na kumweka juu ya kuni, wala sitatia moto chini. Nanyi ombeni kwa jina la mungu wenu, nami nitaomba kwa jina la Bwana; na Mungu yule ajibuye kwa moto, na awe ndiye Mungu. Watu wote wakajibu wakasema, Maneno haya ni mazuri.”                              

 

Ubatizo wa Roho Mtakatifu.

Fahamu ya kuwa anayebatiza kwa Roho Mtakatifu Ni Bwana Yesu mwenyewe, Na ubatizo huu ni mpango wa Mungu, ni ahadi ya Mungu kwa waaminio kwa hiyo kila mmoja anastahili kupokea kwa Imani na kufungua moyo wake kuhakikisha kuwa maisha yake yanajaa na kufunikwa na uwepo wa Mungu Roho Mtakatifu sawa na neno lake lisemavyo:-

 

a.       Mathayo 3:11 “Kweli mimi nawabatiza kwa maji kwa ajili ya toba; bali yeye ajaye nyuma yangu ana nguvu kuliko mimi, wala sistahili hata kuvichukua viatu vyake; yeye atawabatiza kwa Roho Mtakatifu na kwa moto.”

 

b.       Ubatizo huu ni ahadi ya Mungu mwenyewe kwa kila mtu amwaminiye

Yoel 2:28 “Hata itakuwa, baada ya hayo, ya kwamba nitamimina roho yangu juu ya wote wenye mwili; na wana wenu, waume kwa wake, watatabiri, wazee wenu wataota ndoto, na vijana wenu wataona maono;”

               

Luka 24:49 “Na tazama, nawaletea juu yenu ahadi ya Baba yangu; lakini kaeni humu mjini, hata mvikwe uwezo utokao juu.”

 

Matendo 2:38-39 “Petro akawaambia, Tubuni mkabatizwe kila mmoja kwa jina lake Yesu Kristo, mpate ondoleo la dhambi zenu, nanyi mtapokea kipawa cha Roho Mtakatifu. Kwa kuwa ahadi hii ni kwa ajili yenu, na kwa watoto wenu, na kwa watu wote walio mbali, na kwa wote watakaoitwa na Bwana Mungu wetu wamjie.”

 

c.       Lazima uwe na nia ya kutumika – Ubatizo wa Roho Mtakatifu ni kwaajili ya utumishi, Roho wa Mungu anatabia ya kutaharakisha watu kwaajili ya utumishi, Pale tunapokuwa tayari kwa huduma na kukubali kutumika huku na huko Roho Mtakatifu atakuwa radhi nasi, Ubatizo huu hauwafai watu ambao wakataa tu, unawafaa watu ambao wako tayari kwa kazi kwa sababu Roho Hatakupa kutulia

 

Waamuzi 13:24-25 “Basi yule mwanamke akamzaa mtoto mwanamume akamwita jina lake Samsoni, mtoto huyu akakua, Bwana akambarikia. Roho ya Bwana ikaanza kumtaharakisha katika Mahane-dani, katikati ya Sora na Eshtaoli.”

 

Yeremia 47:6-7 “Ee upanga wa Bwana, Siku ngapi zitapita kabla hujatulia? Ujitie katika ala yako; Pumzika, utulie. Utawezaje kutulia, Ikiwa Bwana amekupa agizo? Juu ya Ashkeloni na juu ya pwani, Ndipo alipoyaamuru hayo.”

 

d.       Kwa maombi bila kuchoka – Kama itatokea hujabatizwa katika Roho mtakatifu wakati Fulani huo usiwe mwisho au mwanzo wa kukata tamaa maandiko yanatutia moyo kuendelea kung’ang’ania mpaka tumpokee Roho Mtakatifu, aidha huwezi kupokea Roho Nyingine zaidi ya kile unachokiomba, iko dhana ya watu kufikiri kuwa ukiwekewa mikono wakati wa maombi utapokea roho Nyingine, Mungu atakupoa sawasawa na kuomba kwako

 

Luka 18:9-13 “Nami nawaambia, Ombeni, nanyi mtapewa; tafuteni, nanyi mtaona; bisheni, nanyi mtafunguliwa. Kwa kuwa kila aombaye hupokea; naye atafutaye huona; naye abishaye atafunguliwa. Maana ni yupi kwenu aliye baba, ambaye mwanawe akimwomba mkate, atampa jiwe au samaki, badala ya samaki atampa nyoka? Au akimwomba yai, atampa nge? Basi, ikiwa ninyi mlio waovu mnajua kuwapa watoto wenu vipawa vyema, je! Baba aliye mbinguni hatazidi sana kuwapa Roho Mtakatifu hao wamwombao?

 

e.       Lazima uwe na imani

Maswala yote ya kiroho yanapokelewa kwa Imani, wakati wote mtu akiwa na mashaka hawezi kupokea kitu kutoka kwa Mungu, kwani pasipo Imani haiwezekani kumpendeza Mungu, kwa hiyo Mtu anayemuhitaji Roho wa Mungu ni lazima aombe kwa Imani,

 

Waebrania 11:6 “Lakini pasipo imani haiwezekani kumpendeza; kwa maana mtu amwendeaye Mungu lazima aamini kwamba yeye yuko, na kwamba huwapa thawabu wale wamtafutao.”

 

Wagalatia 3:2 “Nataka kujifunza neno hili moja kwenu. Je! Mlipokea Roho kwa matendo ya sheria, au kwa kusikia kunakotokana na imani?

 

f.         Kuna umuhimu wa kuomba kwa kupaaza sauti – watu wanaoomba kimyakimya maombi ya ubatizo wa Roho Mtakatifu ni vigumu sana kujazwa maandiko yanaonyesha kuwa wale waliobatizwa katika Roho Mtakatifu walikuwa wakiomba kwa sauti ya kusikika kubwa na ndio maana walijazwa na wakasikika wakisema kwa lugha nyingine

Zaburi 81:10 “Mimi ndimi Bwana, Mungu wako, Niliyekupandisha toka nchi ya Misri; Fumbua sana kinywa chako nami nitakijaza.”

 

Matendo 10:45-46 “Na wale waliotahiriwa, walioamini, wakashangaa, watu wote waliokuja pamoja na Petro, kwa sababu Mataifa nao wamemwagiwa kipawa cha Roho Mtakatifu. Kwa maana waliwasikia wakisema kwa lugha, na kumwadhimisha Mungu. Ndipo Petro akajibu,”

 

Kwa hiyo baada ya kujifunza namna hii na kusikia neno la Mungu kuhusu Ubatizo wa Roho Mtakatifu unapaswa kuamini na kuyatendea kazi yale yote ambayo umeyasikia na ninakuhakikishia hutakuwa kama ulivyo.

Yesu alisisitiza juu ya ahadi hii ya ujio wa Roho Mtakatifu kwa sababu

Roho Mtakatifu ni Msaidizi mwingine, Roho Mtakatifu ana uwezo wa kubadilisha maisha, Roho Mtakatifu hutuvika uwezo au Nguvu kutoka juu, Roho Mtakatifu atatuongoza katika kweli yote Roho Mtakatifu humshuhudia Yesu Kristo, Roho Mtakatifu hutoa nyenzo za kutendea kazi, Roho Mtakatifu ni njia ya kurahisisha ukomavu wa kiroho, Roho Mtakatifu hutupa hekima ya utawala na maamuzi, Roho Mtakatifu hutupa nguvu za kukabiliana na uchawi, kuna na mambo mengine mengi sana ambayo kibinadamu hatuwezi kuyatakeleza bila msaada wa Roho Mtakatifu hivyo ubatizo wa Roho Mtakatifu unabaki kuwa nyenzo Muhimu sana kwa kanisa tangu jana leo na hata milele. Uongezewe neema unapochukua majukumu ya kulitendea kazi neno la Mungu kivitendo, wako katika utumishi.

Na Rev. Innocent Samuel Kamote

Mkuu wa wajenzi Mwenye hekima             

Jumapili, 17 Mei 2026

Kujikwaa kwa watesi wetu na adui zetu!


Zaburi 27:1-3. “Bwana ni nuru yangu na wokovu wangu, Nimwogope nani? Bwana ni ngome ya uzima wangu, Nimhofu nani? Watenda mabaya waliponikaribia, Wanile nyama yangu, Watesi wangu na adui zangu, Walijikwaa wakaanguka. Jeshi lijapojipanga kupigana nami, Moyo wangu hautaogopa. Vita vijaponitokea, Hata hapo nitatumaini.”


Utangulizi:

Ni muhimu kufahamu kuwa Neno la Mungu yaani maandiko matakatifu yanakiri kupitia mwandishi wa zaburi hii ya kuwa Bwana akiwa nuru na wokovu wetu, haijalishi kuwa maadui zetu na watesi wetu hata wawe wengi kiasi gani na hata wajipange vipi, watajikwaa na kuanguka, hii maana yake ni kuwa kumtegemea Mungu kunasababisha tuendelee kubaki wenye nguvu hata kama kuna mashambulizi makali ya adui kutoka kila kona, Zaburi hii pia inafunua Nguvu za Mungu ambazo maadui walipaswa kujiuliza kwanza katika mipango yao kuwa Mungu yuko na nani kabla ya kuanza kujipanga dhidi yetu kwa mashambulizi yoyote yale, Hakuna mtu mwenye hati miliki ya Mungu ati!

2Samuel 5:17-18 “Na hao Wafilisti waliposikia kwamba wamemtia Daudi mafuta ili awe mfalme juu ya Israeli, Wafilisti wote wakapanda kumtafuta Daudi; naye Daudi akapata habari, akashuka akaenda ngomeni. Basi Wafilisti walikuwa wamekuja na kujitawanya bondeni mwa Warefai. Basi Daudi akauliza kwa Bwana, akisema, Je! Nipande juu ya Wafilisti? Utawatia mkononi mwangu? Naye Bwana akamwambia Daudi, Panda; kwa kuwa hakika nitawatia Wafilisti mikononi mwako.”

Ni makosa makubwa sana kupigana vita, kupanga maovu, na kumshambulia kumsema vibaya na kumchafua, mtu ambaye hujui kama ana Mungu au hana, katika vita vya kiroho ni lazima ujue kuwa unayepigana naye ni mwenye haki au mwovu, kama unayepigana naye Mungu yuko upande wake utakufa vibaya, utasambaratika, utaporomoka, utafutika  na hautakuwepo tena kwa kosa la kipuuzi kama hilo lisilozingatia kanuni na utendaji wa Mungu! Watakatifu waliotutangulia Hasa Daudi ambaye alikuwa mtaalamu wa vita alijifunza kuwa Bwana akiwa upande wako atakusaidia, na wanaokuchukia watashindwa na kusambaratika vibaya, Historia yao itafifia na watatoweka duniani!

Zaburi 118:6-8 “Bwana yuko upande wangu, sitaogopa; Mwanadamu atanitenda nini? Bwana yuko upande wangu, msaidizi wangu, Kwa hiyo nitawaona wanaonichukia wameshindwa. Ni heri kumkimbilia Bwana Kuliko kuwatumainia wanadamu.”

Leo basi kwa uzito mkubwa tutatafakari pamoja somo hili muhimu lenye kichwa Kujikwaa kwa watesi wangu na adui zangu, ambalo linakazia ushindi wa ajabu unaowapata watu wa Mungu dhidi ya adui zao, na tutajifunza somo hili kwa kuzingatia vipengele vitatu muhimu vifuatavyo:-



·         Maana ya kujikwaa kwa watesi.

·         Siri ya kujikwaa kwa watesi wetu na adui zetu.

·         Kujikwaa kwa watesi wetu na adui zetu!


Maana ya kujikwaa kwa watesi.

Zaburi 27:1-3. “Bwana ni nuru yangu na wokovu wangu, Nimwogope nani? Bwana ni ngome ya uzima wangu, Nimhofu nani? Watenda mabaya waliponikaribia, Wanile nyama yangu, Watesi wangu na adui zangu, Walijikwaa wakaanguka. Jeshi lijapojipanga kupigana nami, Moyo wangu hautaogopa. Vita vijaponitokea, Hata hapo nitatumaini.”

Ni muhimu kufahamu kuwa neno linalotumika katika Lugha ya Kiebrania kuelezea watesi ni “Tzoreri” au “Oyevai” ambalo kwa Kiingereza ni enemies au oppressors, au adversaries, Maadui, watesaji, watu wanaotaka kukusababishia mabaya katika maisha au wanaofurahia wewe upatwe na mabaya au wanaopanga mipango mibaya juu yako na wenye kutaka kuchafua au kuharibu kibali ulichonacho  hawa ndio wanaitwa watesi an maadui watu ambao hawakufurahii na wanakupinga hawataki mafanikio yako au wanaogopa wewe kufanikiwa hawa Bwana ameahidi katika neno lake kuwa wanapodhamiria kukufanyia mambo yao au hata kama watafanya mambo yao hatimae watajikwaa

Kujikwaa hasa ni nini? Neno linalotumika kuelezea kujikwaa katika lugha ya Kiebrania ni “Kāshal” ambalo maana yake ni kudhoofishwa, kupoteza nguvu, kurudishwa nyuma, kushindwa kusimama, kukutana na kizuizi, kukutana na kikwazo, kukosa uwiano, kuzimia chini ya shinikizo, kuanguka kwa namna isiyotegemewa kwa kiingereza “stumble” au “Fall” kwa hiyo mtu awaye yote anayepambana na watu wa Mungu au mtu wa Mungu anaweza akaanguka na asiinuke tena, huku sio tu kujikwaa kimwili, lakini ni kuanguka kwa mfumo mzima wa adui, kusambaratika kwa mipango, na mifumo ya utendaji wa maadui kupitia nguvu na msaada wa Mungu kwa mtumishi wake.

Zaburi 18:36-40 “Umezifanyizia nafasi hatua zangu, Na miguu yangu haikuteleza. Nitawafuatia adui zangu na kuwapata, Wala sitarudi nyuma hata wakomeshwe. Nitawapiga-piga wasiweze kusimama, Wataanguka chini ya miguu yangu. Nawe hunifunga mshipi wa nguvu kwa vita, Hunitiishia chini yangu walioniondokea. Naam, adui zangu umewafanya wanipe visogo, Nao walionichukia nimewakatilia mbali.”

Siri ya kujikwaa kwa watesi wetu na adui zetu

Neno la Mungu linafunua siri kubwa ni kwa nini maadui hawakufanikiwa, kwanza maadui hawa walikuwa na chuki kubwa na ya kiwango cha juu, walikuwa wamekusudia kuharibu kabisa au kufutilia mbali hawa hawakuwa maadui wa kawaida bali watu waliodhamiria mabaya na katika kudhamiria kwao mabaya walikuwa kama watu wanaokaribia kula nyama kwa uchu hii ni lugha ya kuonyesha tamaa mbaya ya kusababisha uharibifu mkubwa kwa mtu au watu wa Mungu. Walikuwa ni watesi waliokusudia mabaya lakini walijikwaa, Mipango yao iliharibika, uharibifufu uliwapata kwa ghafla, hofu iliwaingia, akili zao zilipigwa na wakachanganyikiwa, maamuzi yao yaligeuzwa kuwa makosa, roho zao ziliingia hatiani, dhamiri zao ziliwasuta, ushindi wako mtu wa Mungu utageuka kuwa ushuhuda kwao, Mwandishi anaeleza kuwa yeye Bwana ni Nuru yake na wokovu wake, haogopi

Zaburi 27:1-3 “Bwana ni nuru yangu na wokovu wangu, Nimwogope nani? Bwana ni ngome ya uzima wangu, Nimhofu nani? Watenda mabaya waliponikaribia, Wanile nyama yangu, Watesi wangu na adui zangu, Walijikwaa wakaanguka. Jeshi lijapojipanga kupigana nami, Moyo wangu hautaogopa. Vita vijaponitokea, Hata hapo nitatumaini.”

Mungu anapokuwa upande wako hakuna anayeweza kusimama kinyume na wewe, adui awaye yote anapokukaribia anakutana na nguvu za Mungu zisizokuwa za kawaida na bila kujielewa wanaanza kupoteza mwelekeo, Mungu hakuwahi kuacha watu wake waonewe, kila anayejipanga kupigana na mtu wa Mungu atashughulikiwa mpaka wajue ya kuwa wewe una Mungu, kama walidhani wao ndio wana Mungu basi Mungu ataonyesha ni kina nani aliwachagua kwaajili ya utukufu wake, adui watapata somo kali ambalo watasimuliana kizazi na kizazi wataelewa ya kuwa kushindana na Mungu ni kujitafutia kifo, ni kupoteza umaarufu, ni kuangamia na kupotea, ni kujifuta katika ramani ya dunia

Zaburi 103:14-15 “Hakumwacha mtu awaonee, Hata wafalme aliwakemea kwa ajili yao. Akisema, Msiwaguse masihi wangu, Wala msiwadhuru nabii zangu.”

Isaya 54:14-17 “Utathibitika katika haki; utakuwa mbali na kuonewa, kwa maana hutaogopa; na mbali na hofu, kwa maana haitakukaribia. Tazama, yamkini watakusanyana; lakini si kwa shauri langu. Watu wo wote watakaokusanyana juu yako wataanguka kwa ajili yako.Tazama, nimemwumba mhunzi avukutaye moto wa makaa, akatoa silaha kwa kazi yake; nami nimemwumba mharibu ili aharibu. Kila silaha itakayofanyika juu yako haitafanikiwa na kila ulimi utakaoinuka juu yako katika hukumu utauhukumu kuwa mkosa. Huu ndio urithi wa watumishi wa Bwana, na haki yao inayotoka kwangu mimi, asema Bwana.”

1Samuel 2:9-10 “Yeye atailinda miguu ya watakatifu wake; Bali waovu watanyamazishwa gizani, Maana kwa nguvu hakuna atakayeshinda; Washindanao na Bwana watapondwa kabisa; Toka mbinguni yeye atawapigia radi; Bwana ataihukumu miisho ya dunia; Naye atampa mfalme wake nguvu, Na kuitukuza pembe ya masihi wake.”                           

Kujikwaa kwa watesi wangu na adui zangu!

Maandiko yanatuthibitishia ya kwamba kila mtu anayekukusudia mabaya juu yako au anayekukaribia kwa nia ovu Mungu atampa kupoteza mwelekeo, wanaopanga mabaya dhidi yako watakosea hatua zao, wanaotaka kukuangusha au kukupoteza wao ndio watakaopotea, hii ni sheria ya kiroho kama Mungu yuko upande wako, adui anapokuja na kukushambulia au kukukaribia ataharibiwa na uwepo wa Mungu, hili sio tukio la bahati mbaya ni tukio la uhakika, wewe na mimi tutamshukuru Mungu kwaajili ya matendo yake makuu atakayotutendea na anayoendela kuyafanya akihukumu kwa haki dhidi ya wale wanaotuchukia, na kujipanga kinyume nasi wao na kila anachojivunia itakuwa historia  

Zaburi 9:1-4 “Nitamshukuru Bwana kwa moyo wangu wote; Nitayasimulia matendo yako yote ya ajabu;Nitafurahi na kukushangilia Wewe; Nitaliimbia jina lako, Wewe Uliye juu. Kwa sababu adui zangu hurudi nyuma; Hujikwaa na kuangamia mbele zako. Kwa maana umenifanyia hukumu na haki Umeketi kitini pa enzi ukihukumu kwa haki.”

Rev. Innocent Samuel Kamote

Mkuu wa wajenzi mwenye Hekima