Mwanzo 21:14-20 “Ibrahimu akaamka asubuhi
na mapema akatwaa mkate na kiriba cha maji, akampa Hajiri akimtwika begani
pake, na kijana, akamruhusu; naye akatoka, akapotea katika jangwa la
Beer-sheba. Yale maji yakaisha katika kiriba, akamlaza kijana chini ya kijiti
kimoja. Akaenda akakaa akimkabili, mbali naye kadiri ya mtupo wa mshale; maana
alisema, Nisimwone kijana akifa; naye akakaa akimkabili, akapaza sauti yake,
akalia. Mungu akasikia sauti ya kijana. Malaika wa Mungu akamwita Hajiri kutoka
mbinguni, akamwambia, Una nini, Hajiri? Usiogope, maana Mungu amesikia sauti ya
kijana huko aliko. Ondoka, ukamwinue kijana, ukamshike mkononi mwako, kwa kuwa
nitamfanya kuwa taifa kubwa. Mungu akamfumbua macho, naye akaona kisima cha maji;
akaenda akakijaza kiriba maji, akamnywesha kijana. Mungu akawa pamoja na huyo
kijana, naye akakua, akakaa katika jangwa, akawa mpiga upinde.”
Utangulizi:
Kama kuna mojawapo ya matukio
magumu sana duniani ni pamoja na tukio la kukataliwa na baba yako aliyekuzaa,
maumivu ya kukataliwa na baba yanaweza kusababisha jeraha lisiloweza kukoma,
hofu, kukosa kujiamini na kutelekezwa, jambo ambalo linaweza kupunguza kwa
kiwango kikubwa uwezo wa kuwaamini watu, lakini pia linaweza kusababisha msongo
wa mawazo, kushindwa kujitambua na kutokujitosheleza, inahitajika nguvu ya
ziada sana kuweza kuwa kawaida na kuishinda hali ya kukataliwa, Lazima uwe na
kitu cha ziada kuweza kujijenga kuwa unastahili na kujikomboa kutoka katika
maumivu hayo ya kihisia kwani hali hii inazalisha hali ya kutaka kujithibitisha.
Haya ndiyo yaliyomkuta Ishmael
baada ya kufukuzwa nyumbani kwa baba yake ambaye kimsingi alikuwa tajiri sana
wa mifugo fedha na dhahabu, lakini inaelezwa kuwa Ishamel na mama yake
walitolewa mikono mitupu, wakipewa maji na mkate tu na hawakuwa hata na mtu wa
kuwasindikiza, wala hawakuwa na chakula hata cha akiba, bali tupu.
Mwanzo 13:21-3 “Abramu akapanda kutoka
Misri, yeye, na mkewe, na kila alichokuwa nacho, na Lutu pamoja naye, mpaka
kusini. Naye Abramu alikuwa ni tajiri sana kwa mifugo, kwa fedha, na kwa
dhahabu. Akaendelea kusafiri kutoka kusini mpaka Betheli, mahali pale
palipokuwapo hema yake kwanza kati ya Betheli na Ai;”
Abrahamu alikuwa ni mtu
aliyefanikiwa sana, alikuwa na makundi makubwa ya mifugo, wasimamizi,
wafanyakazi, utajiri mkubwa wa fedha na dhahabu, lakini alikuwa ni mtu mwenye
jeshi kali lililoweza kupigana vita na wafalme wakubwa katika vita, na moja ya
vita maarufu aliyopigana na kuteka nyara ni vita iitwayo “opereshini Lutu”, ambapo alikwenda kupigana kumuokoa Lutu, Jeshi
hilo lilikuwa na makomandoo 318
ambao walikuwa wamefunzwa vizuri
Mwanzo 14:5-16 “Na mwaka wa kumi na nne
akaja Kedorlaoma na wafalme waliokuwa pamoja naye, wakawapiga Warefai katika
Ashteroth-karnaimu, na Wazuzi katika Hamu, na Waemi katika Shawe-kiryathaimu,na
Wahori katika mlima wao Seiri, mpaka Elparani iliyo karibu na jangwa. Kisha
wakarudi wakaja mpaka Enmisfati, ndio Kadeshi, wakapiga nchi yote ya Waamaleki,
na Waamori waliokaa Hasason-tamari. Mfalme wa Sodoma, na mfalme wa Gomora, na
mfalme wa Adma, na mfalme wa Seboimu, na mfalme wa Bela, ndio Soari, wakatoka
wakapanga vita panapo bonde la Sidimu; wapigane na Kedorlaoma mfalme wa Elamu,
na Tidali mfalme wa Goimu, na Amrafeli mfalme wa Shinari, na Arioko mfalme wa Elasari,
wafalme wanne juu ya wale watano. Na bonde la Sidimu lilikuwa limejaa mashimo
ya lami. Nao wafalme wa Sodoma na Gomora wakakimbia, wakaanguka huko, nao
waliosalia wakakimbia milimani. Wakachukua mali zote za Sodoma na Gomora na
vyakula vyao vyote, wakaenda zao. Wakamtwaa Lutu, mwana wa nduguye Abramu,
aliyekaa huko Sodoma, na mali yake, wakaenda zao. Mtu mmoja aliyeponyoka
akaenda, akampasha habari Abramu Mwebrania; naye amekaa panapo mialoni ya
Mamre, yule Mwamori, ndugu ya Eshkoli, na ndugu ya Aneri, na hao walikuwa
wamepatana na Abramu. Abramu aliposikia ya kwamba nduguye ametekwa mateka,
akawapa silaha vijana wake, waliozaliwa katika nyumba yake, watu mia tatu na
kumi na wanane, akawafuata mpaka Dani. Akajipanga apigane nao usiku, yeye na
watumwa wake, akawapiga, akawafukuza mpaka Hoba, ulioko upande wa kushoto wa
Dameski. Naye akarudisha mali zote, akamrudisha na Lutu nduguye na mali zake,
na wanawake pia, na watu.”
Kwa hiyo unapata picha jinsi
Abrahamu alivyokuwa mtu mkubwa sana mwenye uwezo mwingi na utajiri na mtu
mwenye kumiliki Jeshi lake binafsi, na alipigana na wafalme zaidi ya watano na
kuwashinda na kumrejesha Lutu na familia yake nyumbani na mifugo na mali zake
sasa anamfukuza mtoto wa kumzaa mwenyewe tena mikono mitupu! Kwa mujibu wa vitabu vya mafafanuzi ya kiyahudi na tamaduni
zake viitwavyo “Talmudi” na “Midrashi” vinaeleza hivi kwa lugha ya
kiingereza kuhusu Ishamel “Ishmael’s
experience upon being sent away by Abraham was one of severe trauma,
desperation and existential abandonment” kwa tafasiri yangu isiyo rasmi
wanasema swala la kufukuzwa kwa Ishmael na
Abrahimu lilikuwa ni mojawapo ya tukio baya, la kusikitisha, na kutelekezwa
kikatili, kusikokuwa kwa kawaida” mtu tajiri mwenye uwezo mkubwa usiokuwa
wa kawaida anamtoa mtoto wake wa kumzaa mikono mitupu bila kujali hali yake ya
baadaye itakuwaje hata kama alizaliwa na mjakazi!
Mgogoro ulianza wakati Sara
alipomshuhudia Ishmael akimdhihaki Isaka siku ile alipofanyiwa ibada ya
shukurani kwaajili ya muujiza ule mkubwa wa kuzaliwa kwake Isaka na kuachishwa
kunyonya
Mwanzo 21:6-10 “Sara akasema, Mungu
amenifanyia kicheko; kila asikiaye atacheka pamoja nami. Akasema, N'nani
angemwambia Ibrahimu, Sara atanyonyesha wana? Maana nimemzalia mwana katika
uzee wake. Mtoto akakua, akaachishwa kunyonya; Ibrahimu akafanya karamu kuu
siku ile Isaka alipoachishwa kunyonya. Sara akamwona yule mwana wa Hajiri
Mmisri, ambaye alimzalia Ibrahimu, anafanya dhihaka. Kwa hiyo akamwambia
Ibrahimu, Mfukuze mjakazi huyu na mwanawe, maana mwana wa mjakazi hatarithi
pamoja na mwanangu, Isaka.”
Jambo hili halikumfurahisha
Abraham, hata hivyo Mungu alimwambia Abrahamu afanye kile ambacho Sara ameagiza
Mwanzo 21:11.-12 “Na neno hilo lilikuwa
baya sana machoni pa Ibrahimu, kwa ajili ya mwanawe. Mungu akamwambia Ibrahimu,
Neno hili lisiwe baya machoni pako, kwa ajili ya huyo mwana, na huyo mjakazi
wako. Kila akuambialo Sara, sikiza sauti yake, kwa maana katika Isaka uzao wako
utaitwa.”
Jambo hili linamuweka Ishmael na
mama yake katika wakati mbaya sana sasa wanapitia hali ngumu na ya uchungu
sana, tutaliangalia somo hizi Sauti ya kijana Jangwani kwa kuzingatia vipengele
vitatu vifuatavyo:-
·
Maumivu
ya kukataliwa
·
Sauti ya
kijana huko jangwani
·
Mungu
anamkumbuka kijana huko jangwani
Maumivu ya kukataliwa
Tunawaona Ishmael na mama yake
wakiwa jangwani maji yanawaishia na mkate unamalizika hali ya mauti sasa ndiyo
inayomzunguka mtoto, akiwa ni kijana wa miaka 16 tu ambaye alilelewa maisha ya
kudekezwa kama mtoto pekee nyumbani ghafla maisha yanabadilika na anatupwa
jangwani, moyoni ana maumivu makali ya kutupwa na kukataliwa anajiona kama mtu
asiye na bahati na ambaye amesalitiwa na baba yake na sio hivyo tu
ametelekezwa, Ishmael na mama yake wanachanganyikiwa wamefukuzwa nyumbani nani
kama wanatakiwa kuja kufia jangwani.
Mwanzo 21:14-16 “Ibrahimu akaamka asubuhi
na mapema akatwaa mkate na kiriba cha maji, akampa Hajiri akimtwika begani
pake, na kijana, akamruhusu; naye akatoka, akapotea katika jangwa la
Beer-sheba. Yale maji yakaisha katika kiriba, akamlaza kijana chini ya kijiti
kimoja. Akaenda akakaa akimkabili, mbali naye kadiri ya mtupo wa mshale; maana
alisema, Nisimwone kijana akifa; naye akakaa akimkabili, akapaza sauti yake,
akalia.”
Maji yamekwisha chakula pia
kimeisha ni jambo la kushangaza kuwa wanatupwa hata bila ya chakula cha akiba
na wanapotelea katika jangwa anakabiliwa na kiu anachoka na wamekuwa dhaifu, mama
yake anamuweka katika kichaka cha nyikani anakimbia mbali ili asimuone mtoto wake
anapokata roho ana wasiwasi na hofu ya kuona mauti ikimmaliza mwanae
Kijana anajutia kumdhihaki Isaka
anatambua kosa lake ambalo sasa linamletea mateso, anakuwa imara na anapokea
mabadiliko toba yake inaonekana kwa ushahidi kuwa alimalizana vizuri na baba
yake kwani alielewa upumbavu wake na sasa alimuheshimu Isaka kwa mujibu wa
masimulizi ya marabi wa kiyahudi “Rabbinic
tradition” (Genesis Rabbah)
adhabu hii ilileta toba na mabadiliko makubwa kwani alikuja kumzika baba yake
kwa heshima akiwa na Isaka ona:-
Mwanzo 25:8-10. “Ibrahimu akafariki, naye
akafa katika uzee mwema, mzee sana, ameshiba siku, akakusanyika kwa watu wake.
Isaka na Ishmaeli wanawe wakamzika katika pango ya Makpela, katika shamba la
Efroni bin Sohari Mhiti, lielekealo Mamre. Katika lile shamba alilolinunua
Ibrahimu kwa wazawa Hethi, huko ndiko alikozikwa Ibrahimu na Sara mkewe.”
Ndugu yangu kutelekezwa
hakumaanishi kuwa umefika mwisho wa maisha, kutelekezwa hakumaanishi kuwa Mungu
amemalizana na wewe watu wanaweza kukukataa na kukutelekeza lakini Mungu kamwe
hawezi kufanya hivyo, Mikono yake bado iko wazi na anaweza kukupokea, Jangwa
ndilo linalomfanya mtu kuwa imara na kuacha upumbavu wake, Jangwa lilikuwa eneo
la somo kwa Ishmael, alijifunza kusamehe hakumuwekea kinyongo baba yake Mungu aliisikiliza sauti yake kule
jangwani na alikuwa amemuandalia kisima
kizuri cha maji ambayo yangeokoa uhai wake na kumfanya kuwa kijana shujaa,
Zaburi 34:6-9 “Maskini huyu aliita, Bwana
akasikia, Akamwokoa na taabu zake zote.Malaika wa Bwana hufanya kituo, Akiwazungukia
wamchao na kuwaokoa. Onjeni mwone ya kuwa Bwana yu mwema; Heri mtu yule
anayemtumaini. Mcheni Bwana, enyi watakatifu wake, Yaani, wamchao hawahitaji
kitu.”
Sauti ya kijana huko jangwani
Mwanzo 21:17-21 “Mungu akasikia sauti ya
kijana. Malaika wa Mungu akamwita Hajiri kutoka mbinguni, akamwambia, Una nini,
Hajiri? Usiogope, maana Mungu amesikia sauti ya kijana huko aliko. Ondoka,
ukamwinue kijana, ukamshike mkononi mwako, kwa kuwa nitamfanya kuwa taifa
kubwa. Mungu akamfumbua macho, naye akaona kisima cha maji; akaenda akakijaza
kiriba maji, akamnywesha kijana. Mungu akawa pamoja na huyo kijana, naye
akakua, akakaa katika jangwa, akawa mpiga upinde. Akakaa katika jangwa la
Parani; mama yake akamtwalia mke katika nchi ya Misri.”
Jina Ishmael maana yake Mungu
amesikia kilio changu, Mungu alisikia kilio cha mtoto, Mungu sio dhalimu hata
pale inapoonekana kuwa ndoto zako zimezikwa na unabii kukuhusu umefukiwa katika
mchanga, Mungu ataendelea kuwa mwaminifu kwa watu wake na neno lake mbingu
ziliitikia sauti jangwani, kijana kweli alikuwa amefukuzwa nyumbani lakini
hakuwa amefukuzwa kutoka kwenye uwepo wa Mungu, Mungu alimwambia Hajiri
usiogope, na Mungu aliyafunua macho yake na akaona kisima chenye maji, kisima
ambacho kimsingi kilikuwapo pale tayari,
watu wengi sio kuwa Mungu amewaacha bali watu wengi wamefungwa macho wasione
fursa na ndio maana wanalia, Ni kazi ya Roho wa Mungu kukufunulia fursa, hauna
sababu ya kulia lakini unapaswa kuinua macho yako uone.
Unaweza kukataliwa, kuteswa na
kufukuzwa na hata kuwekwa nje ya mtandao “Systems” unaweza kutupwa na baba yako
wa kiroho kabisa na unaweza usijaliwe na wale waliotakiwa kukujali lakini hili
ndio tunalojifunza kuwa kama Mungu nanaweza kusikia kilio jangwani taabu yako
haiwezi kunyamaziwa mbinguni, inaweza kunyamaziwa na wanadamu lakini Mungu
hawezi kunyamaza, unaweza kufukuzwa, unaweza kuwa na kiu na unaweza hata
kusahaulika , lakini Mungu hawezi kuacha kukusikia, utembeleo wa malaika
hauzuiliki na hali, na uhakika wa maisha yako ya baadae uko mikononi mwa Mungu,
maji yanaweza kuisha, mkate unaweza kumalizika, milango inaweza kufunga na watu
wanaweza kukaa kimya lakini Mungu anayemsikiliza Ishmael yuko hata leo yeye
hatakuacha ufie jangwani atakufunulia macho yako na atakuelekeza nini cha
kufanya, Mungu alikuwa pamoja na Ishamel Mungu hana upendeleo haijalishi wewe
ni wa mwanamke muungwana au wa mjakazi.
Mungu anamkumbuka kijana huko jangwani
Mungu alikumbuka agano lake
alilolifanya na mama yake kuhusu kijana aliahidi kuwa angemfanya taifa kubwa na
kwa sababu hiyo kufa jangwani haukuwa mpango wa Mungu, Mungu alikumbuka mpango
wake na Mungu alisikia kilio cha Ishmael Mungu akamkumbuka kijana huko
jangwani!
Mwanzo 16:6-11 “Naye Abramu akamwambia
Sarai, Tazama, mjakazi wako yu mkononi mwako, mtendee lililo jema machoni pako.
Sarai akamtesa, naye akakimbia kutoka mbele yake. Malaika wa BWANA akamwona
kwenye chemchemi ya maji katika jangwa, chemchemi iliyoko katika njia ya
kuendea Shuri. Akamwambia, Hajiri, wewe mjakazi wa Sarai, unatoka wapi, nawe
unakwenda wapi? Akanena, Nakimbia mimi kutoka mbele ya bibi yangu Sarai.
Malaika wa BWANA akamwambia, Rudi kwa bibi yako, ukanyenyekee chini ya mikono yake.
Malaika wa BWANA akamwambia, Hakika nitauzidisha uzao wako, wala hautahesabika
kwa jinsi utakavyokuwa mwingi. Malaika wa BWANA akamwambia, Tazama! Wewe una
mimba, utazaa mwana wa kiume, nawe utamwita jina lake Ishmaeli, maana BWANA
amesikia kilio cha mateso yako.”
Mungu alizungumza na Hajiri
wakati wa changamoto, Mungu huleta ufumbuzi wakati wa changamoto, Mungu
alimwambia asiogope, na Mungu alimfunulia macho kuona kisima cha maji, Mungu
alikuwa ameahidi kumfanya Ishamel kuwa taifa kubwa na Ishamel akawa mkuu mno na
wafalme 12 walitokea katika viuno vyake
Mwanzo 25:12-17 “Hivi ndivyo vizazi vya
Ishmaeli, mwana wa Ibrahimu, ambaye Hajiri, Mmisri, mjakazi wa Sara, alimzalia
Ibrahimu. Na haya ndiyo majina ya wana wa Ishmaeli, kwa majina yao, na kwa
vizazi vyao. Mzaliwa wa kwanza wa Ishmaeli, ni Nebayothi, na Kedari, na
Abdeeli, na Mibsamu, na Mishma, na Duma, na Masa, na Hadadi, na Tema, na
Yeturi, na Nafishi, na Kedema. Hao ndio wana wa Ishmaeli, na hayo ni majina
yao, katika miji yao, na katika vituo vyao, maseyidi kumi na wawili kwa kufuata
jamaa zao. Na hii ndiyo miaka ya maisha ya Ishmaeli, miaka mia na thelathini na
saba. Akakata roho, akafa, akakusanyika kwa watu wake.”
Mungu ndiye anayeshikilia maisha
yako, mipango yako iko katika mikono yake tangu kuwekwa kwa misingi ya ulimwengu,
hakuna bahati mbaya yeye ni muumba mwenye upendo, kila mtu duniani yuko katika
mpango wake na ni yeye ndiye anayeziongoza njia zako, na makusudi yake kwako
atayatimiza mwenyewe katika mpango wake haijalishi ni vikwazo gani utakutana
navyo au ni giza gani liko mbele yako hiyo haimaanishi kuwa Mungu amekuacha ni
swala la kufumba na kufumbua tu amini mchakato wa Mungu “trust the process” yeye atakulinda, atakuongoza atakuweka katika njia
iliyo sahihi, hakuna anayeweza kuuzuia mpango wake wala makusudi yake, Mungu
anaweza kuwainua watu kwaajili yako na wakakutendea mema watakusaidia kulifikia
kusudi lako haijalishi watu wamekuchezea kiasi gani lakini Mungu ni mwenye nguvu
kuliko wao, Je uko kwenye jangwa gani? Mungu anaisikia sauti yako, hutafia
jangwani yeye bado hajamalizana na wewe, Mungu ana ahadi na wewe na ni lazima
aitimize!
Na Rev. Innocent Samuel Kamote
Mkuu wa wajenzi mwenye Hekima


