Zaburi 42:5-6 “Nafsi yangu, kwa nini
kuinama, Na kufadhaika ndani yangu? Umtumaini Mungu; Kwa maana nitakuja
kumsifu, Aliye afya ya uso wangu, Na Mungu wangu. Nafsi yangu imeinama ndani
yangu, kwa hiyo nitakukumbuka, Toka nchi ya Yordani, na Mahermoni, na toka
kilima cha Mizari.”
Utangulizi:
Ni muhimu kufahamu kuwa ziko
nyakati katika maisha ya mwanadamu na hata watu wa Mungu ambapo tunapitia
vipindi ambavyo nasfi zetu zinainama kwa sababu ya kuzidiwa na maumivu ya kihisia na kiroho, kunakosababishwa na
huzuni, kukata tamaa, kukosa utulivu, kuwa na mashaka kusongwa na mawazo, hofu,
kutokujitosheleza. Misiba na kuwa mbali na nyumbani au kuwa ugenini au uhamishoni, Watakatifu
waliotutangulia wanaonyesha kuwa nao pia katika nyakati tofauti tofauti
walipitia hali hizi za kuzidiwa na mgandamizo wa mawazo, kukosa tumaini, kuhisi
kama Mungu yuko mbali nao na kuelemewa na changamoto za maisha na upweke na
hivyo kusababisha nafsi zao kuinama. Kutokana na hali hizo wakati mwingine
waliziuliza nafsi zao maswali makali kwanini nafsi yangu unainama ilihali Mungu
yupo? Kwa nini kufadhaika? Wakati Mungu ni tumaini lako? Ona;-
Zaburi 43:3-5 “Niletewe nuru yako na kweli
yako ziniongoze, Zinifikishe kwenye mlima wako mtakatifu na hata maskani yako.
Hivyo nitakwenda madhabahuni kwa Mungu, kwa Mungu aliye furaha yangu na shangwe
yangu; Nitakusifu kwa kinubi, Ee MUNGU, Mungu wangu. Nafsi yangu, kwa nini
kuinama, Na kufadhaika ndani yangu? Umtumaini Mungu; Kwa maana nitakuja
kumsifu, Aliye afya ya uso wangu, Na Mungu wangu.”
Nafsi zetu zinaweza kuinama sio
kwa sababu ya changamoto za maisha pekee lakini pia wakati mwingine ile hali ya
maumivu ya kihisia, kiu ya kuhitaji uwepo wa Mungu, ukavu wa kiroho na ile
tamaa ya kutaka uwepo wa Mungu uwe ndani yetu kwa wingi ili tuweze kuzishinda
changamoto za nje kwa hiyo tunajifunza hapo kuwa tunaweza kuzihubiri nafsi zetu
kuzikemea, kusema nazo na kuzitaka nafsi zetu zisivunjike moyo wala
zisifadhaike na badala yake zimtegemee Mungu. tutajifunza somo hili Nafsi yangu
kwa nini kuinama kwa kuzingatia vipengele vitatu muhimu vifuatavyo:-
·
Maana ya
nafsi kuinama.
·
Sababu
zinazopelekea nafsi zetu kuinama.
·
Nafsi
yangu kwa nini kuinama?
Maana ya nafsi kuinama
Zaburi 42:5-6 “Nafsi yangu, kwa nini
kuinama, Na kufadhaika ndani yangu? Umtumaini Mungu; Kwa maana nitakuja
kumsifu, Aliye afya ya uso wangu, Na Mungu wangu. Nafsi yangu imeinama ndani
yangu, kwa hiyo nitakukumbuka, Toka nchi ya Yordani, na Mahermoni, na toka
kilima cha Mizari.”
Ni muhimu kufahamu kuwa neno nafsi
iliyoinama katika lugha ya Kiebrania inasomeka kama “Shachach Nephesh” misamiati ambayo kwa Kiingereza inasomeka kama “downcast soul”, “discouraged soul”, “Depressed
within me” au “overwhelmed soul” maana
zake kwa Kiswahili ni nasfi iliyovunjika,
nafsi iliyokata tamaa, au nafsi
iliyolemewa na mawazo, nafsi iliyopoteza tumaini au nafsi iliyozidiwa na kuelemewa au nafsi inayopoteza nguvu na ujasiri, nasfi
ya mtu ikiinama ni ukweli ulio wazi kuwa nguvu zote zinaisha na unapoteza kiu
na shauku ya kufanya lolote, mtu mwenye nasfi iliyoinama anakuwa na changamoto
ya kihisia kimwili na kiroho na wakati mwingine inachangiwa na kutoweka au
kupotea kwa matarajio, kutokujibiwa maombi, mambo kutokuenda sawa na kuwa na
hisia kana kwamba Mungu yuko mbali, upweke
wa kiroho, na kadhalika, kwa ujumla
mwandishi anaonyesha kuwa nafsi yake
imeinama kwa sababu ya kuwa mbali na uwepo wa Mungu, Yeye anaonekana
kuwa mbali na nyumbani, na tena mbali na Nyumba ya Mungu iliyokuwako Yerusalem,
Yeye yu katika chanzo cha mto Jordani katikati ya mlima Hermoni, mahali
paitwapo Mizari mbali na Hekalu la Mungu wa Israel au ukuta ule wa kulia
machozi mahali pa ibada.
Sababu zinazopelekea nafsi zetu kuinama.
Kiu na hisia za kuwa mbali na Mungu – Mwanadamu mwenye akili timamu
anayempenda Mungu anapokuwa na hisia za kuwa mbali na Mungu au kukosa
utoshelevu wa kiibada kwa kweli anakosa amani na kuhisi kupungukiwa, Mwandishi
wa Zaburi hii nyakati za agano la kale alikuwa
mbali na nyumba ya Bwana alikuwa katika sehemu ya chanzo cha mto Jordani mahali
unapoishia mlima Hermoni kaskazini mwa nchi ya Israel na kuanzia kilele cha
Mizari, akiwa huko safarini mbali na
nyumba ya Mungu anahisi upweke na anaona kama Mungu amemuacha, nasfi yake
inaumia, mambo hayaendi na ni kama maombi yanaonekana kutokujibiwa na anakata
tamaa nafsi yake inainama kwa sababu ana kiu na hisia ya kuwa mbali na Mungu kuna namna anakosa muunganiko na Mungu wake
Zaburi 42:8-11 “Mchana Bwana ataagiza
fadhili zake, na usiku wimbo wake utakuwa nami, Naam, maombi kwa Mungu aliye
uhai wangu. Nitamwambia Mungu, mwamba wangu, Kwa nini umenisahau? Kwa nini
ninakwenda nikihuzunika, adui wakinionea? Watesi wangu hunitukana mithili ya
kuniponda mifupa yangu, Pindi wanaponiambia mchana kutwa,Yuko wapi Mungu wako?
Nafsi yangu, kwa nini kuinama, Na kufadhaika ndani yangu? Umtumaini Mungu; Kwa
maana nitakuja kumsifu, Aliye afya ya uso wangu, Na Mungu wangu.”
Mazingira magumu ya maisha – Mwandishi akiwa mbali na nyumba ya
Mungu iliyokuwako Yerusalem anazungukwa na changamoto za maisha na mazingira
magumu, anaomba kwa kulia machozi, lakini ni kama hajibiwi, huku akishutumiwa
na kuhojiwa yuko wapi Mungu wake, anaonewa, anatukanwa maumivu yanaingia mpaka
kwenye mifupa yake, nafsi yake inajikuta inainama, Tunapozungukwa na shida za
kifamilia, ugumu wa maisha, magonjwa na kukosa mahitaji muhimu na kila aina ya
fadhaa haya yote yanaweza kuisababisha nafsi ya mwanadamu kuinama.
Zaburi 42:3-5 “Machozi yangu yamekuwa
chakula changu mchana na usiku, Pindi wanaponiambia mchana kutwa, Yuko wapi Mungu
wako. Nayakumbuka hayo nikiweka wazi nafsi yangu ndani yangu, Jinsi nilivyokuwa
nikienda na mkutano, Na kuwaongoza nyumbani kwa Mungu, Kwa sauti ya furaha na
kusifu, mkutano wa sikukuu. Nafsi yangu, kwa nini kuinama, Na kufadhaika ndani
yangu? Umtumaini Mungu; Kwa maana nitakuja kumsifu, Aliye afya ya uso wangu, Na
Mungu wangu.”
Shinikizo kutoka kwa watu – tunaishi katika dunia ambayo wakati
mwingine watu wanaweza kukuchukia bila sababu, wanasema maneno mabaya dhidi
yako au wanakuzushia, au unakuwa wimbo kwenye vinywa vyao, unakataliwa,
unadharauliwa, unasemwa na kusengenywa kila mahali, maneno ya watu yanakuvunja
moyo unasikia jinsi wanavyokushutumu na kukusimanga na kukusema vibaya
inasababisha shinikizo la maisha na kumvunja vunja mtu wa ndani na nasfi
inainama
Zaburi 42:10-11 “Watesi wangu hunitukana
mithili ya kuniponda mifupa yangu, Pindi wanaponiambia mchana kutwa, Yuko wapi
Mungu wako? Nafsi yangu, kwa nini kuinama, Na kufadhaika ndani yangu? Umtumaini
Mungu; Kwa maana nitakuja kumsifu, Aliye afya ya uso wangu, Na Mungu wangu.”
Kukumbuka nyakati nzuri zilizopita – Kuna nyakati ambapo tunakumbuka
nyakati nzuri tulizokuwa nazo, nyakati za furaha na vicheko, nyakati za amani
na furaha ya moyo, nyakati huru,
Mwandishi ni kama anakumbuka nyakati hizo, alikuwa anaenda Hekaluni tena akiwa
kiongozi wa ibada ulikuwa ni wakati wa furaha lakini sasa wakati huo anaukosa,
unaweza kukumbuka nyakati ambazo ulikuwa uko vizuri, ukilinganisha na hali ya
sasa, mambo yako yalikuwa mazuri, ujana wako ulikuwa bomba na ni kama nyakati hizo
zimepita haraka unakosa yale uliyokuwa ukiyatamani na nafsi yako inainama
Zaburi 42:4-5 “Nayakumbuka hayo nikiweka
wazi nafsi yangu ndani yangu, Jinsi nilivyokuwa nikienda na mkutano, Na
kuwaongoza nyumbani kwa Mungu, Kwa sauti ya furaha na kusifu, mkutano wa
sikukuu. Nafsi yangu, kwa nini kuinama, Na kufadhaika ndani yangu? Umtumaini
Mungu; Kwa maana nitakuja kumsifu, Aliye afya ya uso wangu, Na Mungu wangu.”
Hali ya uchovu wa kiroho – Ziko nyakati ambapo kimsingi mambo
yanapokuwa hayaendi uko mpweke unachoka sana unachoka kuomba, unachoka kusubiri
na unaweza kuchoka hata kupigana vita nafsi inashuka na unamuhitaji Mungu,
nafsi inakosa nguvu na ni mpaka Bwana akutegemeze na kukuinua kutoka hapo
ulipoinama ndipo unapoweza kupenya mwandishi alikuwa anapitia hali hii.
Zaburi 145:13-14 “Ufalme wako ni ufalme wa
zamani zote, Na mamlaka yako ni ya vizazi vyote. Bwana huwategemeza wote
waangukao, Huwainua wote walioinama chini.”
Nafsi yangu kwa nini kuinama?
Mwandishi wa zaburi hii
hakubaliani na hali anayoipitia na badala yake anaihoji nafsi yake kwanini
kuinama? Kwanini upate shida, kwanini uteseke? Kwanini ufadhaike, yeye anaamini
ya kuwa atamsifu Mungu aliye afya ya uso wake, yaani uso wake hautakuja
kukunjamana kamwe, yeye ataendelea kufurahia uzuri wa Bwana kwani anaziona njia
za huzuni kuwa ni swala la Muda tu na
anajua ya kuwa, Mungu huwa hakai kimya wakati nafsi zetu zinapoinama, yeye kama
baba anayejali huwahurumia wamchao na kuwaokoa, Neno la Mungu linaonyesha wazi
kuwa Mungu hutoa faraja ya kipekee pale watu wake wanapochoka na kuelemewa kwa
hivyo badala ya kufikiri kuwa uko peke yako Neno la Mungu linaonyesha kuwa yeye
atajitokeza na kutoa msaada hivyo lazima uikumbushe nafsi yako wajibu wake kwa
Bwana na neno la Mungu linasema nini kukuhusu au kuihusu ili usiiname
unapoikumbusha nafsi yako kuendelea kumtegema Bwana haitokuja itokee ukazimia
kupitiliza:-
1. Anaalika wote waliochoka wanaolemewa wamjie
na kuwa atawapa pumziko na raha nafsini mwao. - Mathayo 11:28-30 “Njoni kwangu, ninyi nyote msumbukao na wenye kulemewa na mizigo,
nami nitawapumzisha. Jitieni nira yangu, mjifunze kwangu; kwa kuwa mimi ni
mpole na mnyenyekevu wa moyo; nanyi mtapata raha nafsini mwenu; kwa maana nira
yangu ni laini, na mzigo wangu ni mwepesi.”
2. Mungu huwapa nguvu wale waliochoka wale wanaomtumaini
kama ilivyokuwa kwa mwandishi wa Zaburi hii - Isaya 40:29-31 “Huwapa nguvu wazimiao, humwongezea nguvu yeye asiyekuwa
na uwezo. Hata vijana watazimia na kuchoka, na wanaume vijana wataanguka; bali
wao wamngojeao Bwana watapata nguvu mpya; watapanda juu kwa mbawa kama tai;
watapiga mbio, wala hawatachoka; watakwenda kwa miguu, wala hawatazimia.”
3. Tunaweza kumuomba Mungu atutie nguvu pale
nafsi zetu zinapochoka na kuelemewa - Zaburi 119:25-28 “Nafsi yangu imeambatana na mavumbi, Unihuishe sawasawa na neno lako.
Nalizisimulia njia zangu ukanijibu, Unifundishe amri zako. Unifahamishe njia ya
mausia yako, Nami nitayatafakari maajabu yako. Nafsi yangu imeyeyuka kwa uzito,
Unitie nguvu sawasawa na neno lako.”
4. Iambie nafsi yako imsubiri Bwana kwa kimya
maana yeye hatakuangusha - Zaburi 62:1-6 “Nafsi
yangu yamngoja Mungu peke yake kwa kimya, Wokovu wangu hutoka kwake. Yeye tu
ndiye mwamba wangu na wokovu wangu, Ngome yangu, sitatikisika sana. Hata lini
mtamshambulia mtu, Mpate kumwua ninyi nyote pamoja? Kama ukuta unaoinama, Kama
kitalu kilicho tayari kuanguka,Hufanya shauri kumwangusha tu katika cheo chake;
Huufurahia uongo. Kwa kinywa chao hubariki; Kwa moyo wao hulaani. Nafsi yangu,
umngoje Mungu peke yake kwa kimya. Tumaini langu hutoka kwake. Yeye tu ndiye
mwamba wangu na wokovu wangu, Ngome yangu, sitatikisika sana.”
5. Iamuru nasfi yako kumuhimidi Bwana na
kutokusahau fadhili zake - Zaburi 103:1-5 “Ee nafsi
yangu, umhimidi Bwana. Naam, vyote vilivyo ndani yangu Vilihimidi jina lake
takatifu. Ee nafsi yangu, umhimidi Bwana, Wala usizisahau fadhili zake zote.
Akusamehe maovu yako yote, Akuponya magonjwa yako yote, Aukomboa uhai wako na
kaburi, Akutia taji ya fadhili na rehema, Aushibisha mema uzee wako, Ujana wako
ukarejezwa kama tai;”
Ikumbushe nafsi yako kuwa
haitakiwi kubaki chini hata kama kuna changamoto za aina gani zinakukabili,
Mungu yuko kwa hiyo kama nafsi yako inaweza kuinama yuko Mungu mwenye uwezo wa
kuiinua, kama nafsi yako inaweza kulia yuko Mungu anayeweza kuifanya ikaimba
sifa, kama nafsi yako inaweza kukata tamaa yuko Mungu mwamba wa wokovu wako
anaweza kuleta tumanini, kama nafsi yako inaweza kusumbuka na kuelemewa yuko
Mungu anayeweza kuleta furaha na kuipa raha nafsi yako, Neno la Mungu
linakutaka umtumainie Bwana na kumsifu hata wakati wa changamoto kali za maisha
inuka acha kuketi chini tunaye Mungu aliye karibu wala hajakuacha yeye ni
kimbilio na nguvu na msaada uonekanao tele wakati wa mateso hivyo hupaswi
kuogopa lolote, hata nchi itetemeke, hata milima itikisike, hata moyo wa bahari
uumuke yuko Mungu ambaye ukimtegemea na kumtumaini Moyo wako hauwezi kufadhaika
kamwe yeye hatakuangusha kamwe
hatakuacha wala hatakupungukia, usikate tamaa, usione kuwa mazingira ni magumu,
Mungu yuko kila mahali sio Yerusalem peke yake uwepo wa Mungu uko hata
mapangoni, hata ukimbizini atakushika, utainuka.
“Mungu yuko hapa, Yesu Kristo naye yuko hapa, Roho wake Mungu yuko hapa na malaika wako hapa,x2 kwa nini
mimi niteseke na hali wewe uko hapa, usiniache
uniguse mana Mungu yuko hapa, kwanini mimi nipate tabu, nidharauliwe na kutupwa
hovyo usiniache uniguse, maana Mungu yuko hapa”
Rev. Innocent Samuel Kamote


