Waamuzi
2:8-13 “Kisha Yoshua mwana wa Nuni, mtumishi wa
Bwana, akafa, naye alipata umri wa miaka mia na kumi. Nao wakamzika katika
mpaka wa urithi wake katika Timnath-heresi, katika nchi ya vilima vilima ya
Efraimu, upande wa kaskazini wa mlima wa Gaashi.Tena watu wote wa kizazi hicho
nao walikusanywa waende kwa baba zao; kikainuka kizazi kingine nyuma yao,
ambacho hakikumjua Bwana, wala hawakuijua hiyo kazi ambayo alikuwa ameitenda
kwa ajili ya Israeli. Wana wa Israeli walifanya yaliyokuwa ni maovu mbele za
macho ya Bwana, nao wakawatumikia Mabaali. Wakamwacha Bwana, Mungu wa baba zao,
aliyewaleta kutoka katika nchi ya Misri, wakafuata miungu mingine, baadhi ya
miungu ya watu wale waliokaa karibu nao pande zote, wakajiinamisha mbele yao;
wakamkasirisha Bwana, akaghadhibika. Wakamwacha Bwana, wakamtumikia Baali na
Maashtorethi.”
Utangulizi:
Mojawapo ya jukumu kubwa la Kanisa
pamoja na mambo mengine ni pamoja na kuwahudumia watoto, Mungu amewapa watoto
kipuambele kikubwa sana na kwa sababu hiyo kuwapuuzia watoto ni kumpuuzia
Mungu, Kanisa lina wajibu wa kuwajenga na kuwahudumia watoto kwa uaminifu
vilevile kama linavyowahudumia watu wazima iko dhana potofu kwa wahudumu wengi
wa injili inayofikiri kuwapuuzia watoto na kutokutaka kuwaleta karibu na Yesu
kufanya hivi ni kufanya makosa makubwa sana ambayo Yesu mwenyewe aliyakemea.
Mathayo
19:13-15 “Ndipo akaletewa watoto wadogo ili aweke
mikono yake juu yao na kuwaombea; wanafunzi wake wakawakemea. Lakini Yesu
akasema, Waacheni watoto wadogo waje kwangu; wala msiwazuie; kwa maana walio
mfano wa hao, ufalme wa mbinguni ni wao. Akaweka mikono yake juu yao, akatoka
huko.”
Kama tunamtumikia Mungu kwa haki na
kweli na kama tunatanguliza maslahi ya ufalme wa mbinguni basi hatutaweza kamwe
kuwaacha nyuma watoto katika mambo ya Mungu ni lazima twende pamoja na wao na
kuwakuza katika neema hii kwani malezi ya wototo wadogo katika njia ya Mungu ni
maagizo ya kibiblia Mithali 22:6 “Mlee mtoto katika njia impasayo, Naye hataiacha, hata
atakapokuwa mzee.”
Kumbukumbu
6:4-9 “Sikiza, Ee Israeli; Bwana, Mungu wetu, Bwana
ndiye mmoja. Nawe mpende Bwana, Mungu wako, kwa moyo wako wote, na kwa roho
yako yote, na kwa nguvu zako zote. Na maneno haya ninayokuamuru leo, yatakuwa
katika moyo wako; nawe uwafundishe watoto wako kwa bidii, na kuyanena uketipo
katika nyumba yako, na utembeapo njiani, na ulalapo, na uondokapo. Yafunge yawe
dalili juu ya mkono wako, nayo yatakuwa kama utepe katikati ya macho yako.Tena
yaandike juu ya miimo ya nyumba yako, na juu ya malango yako.”
Kwa msingi huo wakati huu sisi kama
watendakazi na wahudumu katika shamba la Mungu tutachua muda kujifunza kwa kina
na mapana na marefu kuhusiana na swala zima la huduma ya watoto kwa kuzingatia
vipengele vitatu muhimu vifuatavyo:-
- Umuhimu
wa huduma ya watoto
- Umuhimu
wa walimu wa watoto
- Jinsi
ya kufanikisha huduma ya watoto
Umuhimu
wa huduma ya watoto
Tumeona katika utangulizi wa somo hili
jinsi Mungu alivyowapa watoto kipaumbele watoto, Mungu anataka watoto
wajulishwe njia zake, aliwaamuru Israel kufanya hivyo na kwakweli wao wamekuwa
hodari katika kuhakikisha kuwa watoto wao wanafuata njia zao na imani yao, sisi
nasi kama Kanisa hatuna budi kulishika hili vile vile na kuhakikisha kuwa
hatuwaachi watoto wetu bila ujuzi wa neno la Mungu ili wakue katika njia hii na
imani hii
Zaburi
78:5-7 “Maana alikaza ushuhuda katika Yakobo, Na
sheria aliiweka katika Israeli. Aliyowaamuru baba zetu Wawajulishe wana wao,
Ili kizazi kingine wawe na habari, Ndio hao wana watakaozaliwa. Wasimame na
kuwaambia wana wao Wamwekee Mungu tumaini lao. Wala wasiyasahau matendo ya Mungu,
Bali wazishike amri zake.”
Mungu anaeleza baadae siri ni kwanini
alimchagua Abrahamu, Mungu anasema alimjua Abrahamu kwamba atawafundisha watoto
wake waishike njia yake baada yake na kuwaamuru kutenda haki, Kumbe basi Mungu anapogundua
kuwa tumemaanisha katika kuwahudumia watoto na washirika kwa ujumla
atatufurahia na kuruhusu maelfu ya watu wake waje kwetu akijua ya kuwa watoto
watafundishwa njia za Mungu katika Kanisa letu, Kanisa linalowajali watoto
Mungu hulibariki sana!
Mwanzo
18:18-19 “BWANA akanena, Je! Nimfiche Ibrahimu
jambo nilifanyalo, akiwa Ibrahimu atakuwa taifa kuu, hodari, na katika yeye
mataifa yote ya dunia watabarikiwa? Kwa maana nimemjua ya kwamba atawaamuru
wanawe, na nyumba yake baada yake waishike njia ya BWANA, wafanye haki na hukumu,
ili kwamba BWANA naye akamtimizie Ibrahimu ahadi zake.”
Huduma ya watoto ni kazi maalumu ya
kuujenga ufalme wa Mungu, hii sio huduma ya malezi ya kuwatunza watoto wakati
wazazi wanasali au wako katika ibada, hii ni huduma maalumu ya kumjenga mtoto
kiroho, kimaadili na kitabia, kwa kuushika moyo wake mapema na kumfundisha njia
za Mungu katika hatua za awali kwa lugha, mbinu na njia zitakazowafanya watoto
kuelewa kwa haraka Mithali 22:6 “Mlee mtoto katika njia impasayo, Naye hataiacha, hata
atakapokuwa mzee.”
Endapo kanisa litaacha wajibu huu
muhimu na kuwaacha watenda kazi wake, wanafunzi, wahudumu na wenye hekima
wakiwa hawana ujuzi kuhusu maswala ya watotoni Dhahiri kuwa tunaandaa kizazi
ambacho hakitakuwa kinamjua Mungu kama kile kilichoinuka nyakati za wazee wetu
katika Israel baada ya kufa kwake Yoshua na wakati wa kizazi cha nyakati za
waamuzi ambao walicheza sana na mambo ya hvyo na kuwapa adui zao nafasi ya
kuwaonea na kuwakandamiza
Waamuzi
2:8-12 “Kisha Yoshua mwana wa Nuni, mtumishi wa
Bwana, akafa, naye alipata umri wa miaka mia na kumi. Nao wakamzika katika
mpaka wa urithi wake katika Timnath-heresi, katika nchi ya vilima vilima ya
Efraimu, upande wa kaskazini wa mlima wa Gaashi. Tena watu wote wa kizazi hicho
nao walikusanywa waende kwa baba zao; kikainuka kizazi kingine nyuma yao,
ambacho hakikumjua Bwana, wala hawakuijua hiyo kazi ambayo alikuwa ameitenda
kwa ajili ya Israeli. Wana wa Israeli walifanya yaliyokuwa ni maovu mbele za
macho ya Bwana, nao wakawatumikia Mabaali.Wakamwacha Bwana, Mungu wa baba zao,
aliyewaleta kutoka katika nchi ya Misri, wakafuata miungu mingine, baadhi ya
miungu ya watu wale waliokaa karibu nao pande zote, wakajiinamisha mbele yao;
wakamkasirisha Bwana, akaghadhibika.”
Mungu atupe neema na hekima kizazi cha
leo, tusipuuzie swala hili nyeti linalohusiana na huduma hii ya watoto ili kwa
upendo na kwa masalahi ya ufalme wa Mungu tusimtengenezee Bwana kizazi au Kanisa
la baadae lisilomjua Mungu wala njia zake kwani kwa kufanya hivyo tutakuwa
tunamkosea Bwana hivyo huduma hii ya kuwafudnisha watoto njia za Bwana ni
mapenzi yake, kumbuka neno la Msingi Kikainuka kizazi kingine hapo maana yake
ni kizazi kilichokosa mafundisho, kizazi kisichorithishwa imani, kizazi
kilichokosa uangalizi wa kiroho, kizazi ambacho hakuna mtu anakijali, kizazi
ambacho hata stori kuhusu Mungu na matendo yake makuu hawakuwahi
kuyasikia.
Umuhimu
wa walimu wa watoto
Wahudumu wanaohusika na kuwafundisha
watoto wanapaswa kuwa na uelewa wa kina kuwa wao ni wa muhimu sana kuliko mtu
yeyote yule kwa sababu wao ndio wanaouweka msingi wa mwanzo kabisa wa imani kwa
watoto, wanaipanda mbegu ya imani na uadilifu na kuwajengea watoto tabia njema
na kuwafunda ili wakue na kuwa kama Yesu katika upendo, imani mwenendo na
usafi, wanalazimika kujikoki na kufanya maandalizi ya kutosha na ya kina ili
kuboresha mwenendo mzima wa malezi elekezi
kwa watoto hawa, kwa kufanya hivi wao wanaandaa kile kizazi kijacho cha
watu waliofunzwa na wenye nidhamu ya hali ya juu watakaokuwa nuru na chumvi kwa
ulimwengu ujao.
-
Wao ni
wajenzi wa msingi na ukuaji bora wa watoto kiroho, wanawasaidia
watoto kukua wakiwa imara kiimani na kuhakikisha kuwa msingi huo unadumu siku
zote za maisha yao, hapo tunawatengenezea uwezo wa kusikia na kulitendea kazi
neno la Mungu jambo litakalowafanya wakue wakiwa imara na wenye ujuzi kuhusu Mungu.
Luka
6:47-49 “Kila mtu ajaye kwangu, na kuyasikia maneno
yangu na kuyatenda, nitawaonyesha mfano wake. Mfano wake ni mtu ajengaye nyumba,
na kuchimba chini sana, na kuweka msingi juu ya mwamba; na kulipokuja gharika,
mto uliishukia nyumba ile kwa nguvu, usiweze kuitikisa; kwa kuwa imejengwa
vizuri. Lakini yule aliyesikia ila hakutenda, mfano wake ni mtu aliyejenga
nyumba juu ya ardhi pasipokuwa na msingi, mto ukaishukia kwa nguvu, ikaanguka
mara; na maangamizi yake nyumba ile yakawa makubwa.”
-
Wao ni
warithishaji wa mila na tamaduni za kiimani (Pedagogies) walimu wa
watoto katika Kanisa wanafanya kazi ya kuwaandaa wana wa kifalme kusimama imara
na kuwa hodari katika maneno na matendo
ya kazi zao za kifalme, Nyakati za Biblia watoto wa kifalme walikuwa na waalimu
wao ambao kazi zao zilikuwa ni ni kuwafundisha watoto wa kifalme kwa
kuwarithisha mila miiko na desturi za kifalme ili watakapokuja kuwa wafalme
wasikiuke mila na desturi hizo, wakiwa na uwezo wa kusema na kutenda, au
kufundisha na kufanya.
Matendo
1:1 “Kitabu kile cha kwanza nalikiandika, Theofilo,
katika habari ya mambo yote aliyoanza Yesu kufanya na kufundisha,”
Matendo
7:22 “Musa akafundishwa hekima yote ya Wamisri,
akawa hodari wa maneno na matendo.”
-
Wao ni
wawezeshaji wa kusikia na kutenda Msingi
mkubwa sana wa walimu wa neno la Mungu unakazia katika kusikia na kutenda,
kimsingi kama mtu hajatenda kibiblia humaanisha hajasikia, Mwalimu mzuri na
mwema ni yule aneyewawezesha watoto kusikia kisha wakatenda huu ndio mkazo wa
waalimu wa kibiblia na ndicho wanacho paswa kukifanya walimu wa watoto.
Mathayo
7:24-27 “Basi kila asikiaye hayo maneno yangu, na
kuyafanya, atafananishwa na mtu mwenye akili, aliyejenga nyumba yake juu ya
mwamba; mvua ikanyesha, mafuriko yakaja, pepo zikavuma, zikaipiga nyumba ile,
isianguke; kwa maana misingi yake imewekwa juu ya mwamba.Na kila asikiaye hayo
maneno yangu asiyafanye, atafananishwa na mtu mpumbavu, aliyejenga nyumba yake
juu ya mchanga; mvua ikanyesha, mafuriko yakaja, pepo zikavuma, zikaipiga
nyumba ile, ikaanguka; nalo anguko lake likawa kubwa.”
Yakobo
1:22-25 “Lakini iweni watendaji wa neno, wala si
wasikiaji tu, hali mkijidanganya nafsi zenu. Kwa sababu mtu akiwa ni msikiaji
wa neno tu, wala si mtendaji, mtu huyo ni kama mtu anayejiangalia uso wake
katika kioo. Maana hujiangalia, kisha huenda zake, mara akasahau jinsi alivyo.
Lakini aliyeitazama sheria kamilifu iliyo ya uhuru, na kukaa humo, asiwe
msikiaji msahaulifu, bali mtendaji wa kazi, huyo atakuwa heri katika kutenda
kwake.”
Mathayo
21:28-32 “Lakini mwaonaje? Mtu mmoja alikuwa na
wana wawili; akamwendea yule wa kwanza, akasema, Mwanangu, leo nenda kafanye
kazi katika shamba la mizabibu. Akajibu akasema, Naenda, Bwana; asiende.
Akamwendea yule wa pili, akasema vile vile. Naye akajibu akasema, Sitaki;
baadaye akatubu, akaenda. Je! Katika hao wawili ni yupi aliyefanya mapenzi ya
babaye? Wakamwambia, Ni yule wa pili. Basi Yesu akawaambia, Amin nawaambia,
watoza ushuru na makahaba wanatangulia mbele yenu kuingia katika ufalme wa
Mungu. Kwa sababu Yohana alikuja kwenu kwa njia ya haki, ninyi msimwamini;
lakini watoza ushuru na makahaba walimwamini, nanyi hata mlipoona, hamkutubu
baadaye, ili kumwamini.”
-
Wao ni
chachu ya makuzi ya kiroho Msingi wa ukuaji wa kiroho, kumpenda Mungu
na kumtumikia ni mchakato wa muda mrefu sana unaojumuisha toba, maendeleo ya
kukua kiroho, kiimani na kimafundisho, ili mtoto akue akimpendeza Mungu na
wanadamu anapaswa kuwa na walimu bora wanaojua wanampeleka wapi mtoto, wao
wenyewe wakiwa ndio kielelezo cha ibada, heshima na utumishi, Kanisa hatuna
budi kuwekeza katika mioyo ya watoto kwa mafundisho sahihi, tuwalishe kondoo wa
Mungu bila kujali umri wao au kuwapuuzia.
Yohana
21:15 “Basi walipokwisha kula, Yesu akamwambia
Simoni Petro, Je! Simoni wa Yohana, wewe wanipenda kuliko hawa? Akamwambia,
Naam, Bwana, wewe wajua kuwa nakupenda. Akamwambia, Lisha wana-kondoo wangu.
Akamwambia tena mara ya pili, Simoni wa Yohana, wanipenda? Akamwambia, Ndiyo,
Bwana, wewe wajua kuwa nakupenda. Akamwambia, Chunga kondoo zangu. Akamwambia
mara ya tatu, Simoni wa Yohana, wanipenda? Petro alihuzunika kwa vile
alivyomwambia mara ya tatu, Wanipenda? Akamwambia, Bwana, wewe wajua yote; wewe
umetambua ya kuwa nakupenda. Yesu akamwambia, Lisha kondoo zangu.”
-
Wao huwajengea tabia njema mapema – walimu wa
watoto ndio wanaopanda msingi wa tabia njema mapema, na hata mtu anapokuja kuwa
mtu mzima kimsingi mambo mengi sana yanakuwa yamejengeka tangu utoto, Bibi yake
Timotheo na mama yake licha ya kuwa wazazi lakini pia walikuwa walimu wa awali
wa Imani safi isiyo na unafiki wakiipandikiza hivyo kwa Timotheo na kumfanya
Timitheo kuja kuwa mtu mwenye sifa njema sana miongoni mwa wanafunzi wa nyakati
za kanisa la kwanza, vigezi vulivyomfanya Paulo aambatane naye.
2Timotheo
3:13-15. “lakini watu wabaya na wadanganyaji
wataendelea, na kuzidi kuwa waovu, wakidanganya na kudanganyika. Bali wewe ukae
katika mambo yale uliyofundishwa na kuhakikishwa, kwa maana unajua ni akina
nani ambao ulijifunza kwao; na ya kuwa tangu utoto umeyajua maandiko
matakatifu, ambayo yaweza kukuhekimisha hata upate wokovu kwa imani iliyo
katika Kristo Yesu.”
2Timotheo
1:5-7 “Nami natamani sana kukuona, nikiyakumbuka
machozi yako, ili nijae furaha; nikiikumbuka imani uliyo nayo isiyo na unafiki,
ambayo ilikaa kwanza katika bibi yako Loisi, na katika mama yako Eunike, nami
nasadiki wewe nawe unayo. Kwa sababu hiyo nakukumbusha, uichochee karama ya
Mungu, iliyo ndani yako kwa kuwekewa mikono yangu. Maana Mungu hakutupa roho ya
woga, bali ya nguvu na ya upendo na ya moyo wa kiasi.”
Matendo
16:1-3 “Basi akafika Derbe na Listra, na hapo
palikuwa na mwanafunzi mmoja jina lake Timotheo, mwana wa mwanamke Myahudi
aliyeamini; lakini babaye alikuwa Myunani. Mtu huyo alishuhudiwa vema na ndugu
waliokaa Listra na Ikonio.Paulo akamtaka huyo afuatane naye, akamtwaa
akamtahiri kwa ajili ya Wayahudi waliokuwako pande zile; kwa maana wote walijua
ya kuwa babaye ni Myunani.”
Jinsi
ya kufanikisha huduma ya watoto
Watoto ni urithi wa Mungu, kwa maana
ya kwamba Mungu anataka kuwekeza kwa watoto kwa faida ya ufalme wake na kazi
yake ya baadae wakati ambapo adui naye anakusudia kuwamaliza mapema ili waweze
kutimiza mapenzi yake hapa duniani, kwa msingi huo kama kanisa hatuna budi
kuhakikisha kuwa tunawekeza nguvu zetu mapema ili kujikinga na yale yaliyotokea
wakati wa waamuzi baada ya kifo cha
Yoshua ambako kuliinuka kizazi ambacho hakikumjua Mungu wala matendo yake, Ni
huduma ya watoto ndiyo itakayolinda kizazi kijacho, na bila ya hivyo
tutakatikia sehemu fulani na kuishia hapo, kwa hiyo ni muhimu kwa kila kanisa
na watendakazi na wahudumu wa injili kuhakikisha
tunaifanikisha huduma hii ya watoto kwa
gharama yoyote ile Lazima kila kanisa:
Kuweko
na maono kwa maswala ya watoto Mithali
29:17-18 “Mrudi mwanao naye atakustarehesha; Naam,
atakufurahisha nafsi yako. Pasipo maono, watu huacha kujizuia; Bali ana heri
mtu yule aishikaye sheria.”
Walimu
walioandaliwa vema – Huduma ya walimu wa watoto ni wito maalumu
kabisa sio kila mtu anaweza kuwahudumia watoto, kwa hiyo lazima kuweko mkakati
wa kuwapata na kuwaleta kwa Yesu walimu, waliookoka, wanaowapenda watoto, wenye
mzigo na wenye huduma hii, hata kama wamesomea ualimu wa awali pia lakini wawe
wamejazwa Roho Mtakatifu, wanaopenda watoto, wenye uvumilivu na subira wanaojua
kuchukuliana nao wenye kuomba na wawe mfano wa kuigwa
Waefeso
4:11-12 “Naye alitoa wengine kuwa mitume, na
wengine kuwa manabii; na wengine kuwa wainjilisti na wengine kuwa wachungaji na
waalimu; kwa kusudi la kuwakamilisha watakatifu, hata kazi ya huduma itendeke,
hata mwili wa Kristo ujengwe; hata na sisi sote tutakapoufikia umoja wa imani
na kumfahamu sana Mwana wa Mungu, hata kuwa mtu mkamilifu, hata kufika kwenye
cheo cha kimo cha utimilifu wa Kristo;”
Kuandaliwa
kwa mfumo wa mafundisho yanayofaa - Watoto wana namna yao ya kufundishwa,
zinaweza kutumika hadithi za kibiblia, michoro, michezo yenye ujumbe, mistari
ya kukariri, uimbaji, nyimbo, na lugha inayoendana na umri wao, ikiwa kwa watu
wazima kuna maziwa na chakula kigumu basi ni zaidi sana lazima kuwe na namna
njema ya kuwekeza mafundisho kwa watoto wadogo kulingana na umri wao pia
Waebrania
5:11-14 “Ambaye tuna maneno mengi ya kunena katika
habari zake; na ni shida kuyaeleza kwa kuwa mmekuwa wavivu wa kusikia. Kwa
maana, iwapasapo kuwa waalimu, (maana wakati mwingi umepita), mnahitaji
kufundishwa na mtu mafundisho ya kwanza ya maneno ya Mungu; nanyi mmekuwa
mnahitaji maziwa wala si chakula kigumu. Kwa maana kila mtu atumiaye maziwa
hajui sana neno la haki, kwa kuwa ni mtoto mchanga. Lakini chakula kigumu ni
cha watu wazima, ambao akili zao, kwa kutumiwa, zimezoezwa kupambanua mema na
mabaya.”
Mazingira
salama, uadilifu na ushirikiano na wazazi - Watoto wanahitaji ulinzi na usalama wa
kimwili, kiroho na kihisia, kwa msingi huo ni lazima kanisa lijiwekee kanuni za
ulinzi wa Mtoto, tuwatengenee mazigira rafiki yasiyo na unyanyasaji na
ushirikiano mkubwa na wazazi hatuwezi kuwapata watoto kwa sababu wako chini ya
mamlaka ya wazazi wao kwa hiyo ni lazima wazazi watoe ushirikiano mkubwa ikiwa
ni pamoja na kuwaleta ibadani au kuwaleta katika makusanyiko na makambi ya makongamano
ya watoto, Yusufu na Mariamu hawakuacha kumpeleka Yesu Hekaluni tangu wakati wa
utoto wake, mpaka ikatokea kuwa mtoto huyu akawa anapenda kujifunza neno.
Luka
2:21-24 “Hata zilipotimia siku nane za kumtahiri,
aliitwa jina lake Yesu; kama alivyoitwa na malaika kabla hajachukuliwa
mimba.Kisha, zilipotimia siku za kutakasika kwao, kama ilivyo torati ya Musa
walikwenda naye hata Yerusalemu, wamweke kwa Bwana,(kama ilivyoandikwa katika
sheria ya Bwana, Kila mtoto mwanamume aliye kifungua mimba ya mamaye na aitwe
mtakatifu kwa Bwana),wakatoe na sadaka, kama ilivyonenwa katika sheria ya
Bwana, Hua wawili au makinda ya njiwa wawili”
Luka
2:40-46 “Yule mtoto akakua, akaongezeka nguvu,
amejaa hekima, na neema ya Mungu ilikuwa juu yake. Basi, wazee wake huenda
Yerusalemu kila mwaka, wakati wa sikukuu ya Pasaka. Na alipopata umri wake
miaka kumi na miwili, walipanda kama ilivyokuwa desturi ya sikukuu; na
walipokwisha kuzitimiza siku, wakati wa kurudi kwao, yule mtoto Yesu alibaki
nyuma huko Yerusalemu, na wazee wake walikuwa hawana habari. Nao wakadhani ya
kuwa yumo katika msafara; wakaenenda mwendo wa kutwa, wakawa wakimtafuta katika
jamaa zao na wenzao; na walipomkosa, wakarejea Yerusalemu, huku wakimtafuta.
Ikawa baada ya siku tatu wakamwona hekaluni, ameketi katikati ya waalimu,
akiwasikiliza na kuwauliza maswali.”
Mwisho kabisa maombi ni jambo la
msingi sana kwa huduma hii, kama tunavyojua kila kitu cha kiroho kinahitaji
maombi basi ni muhimu kwetu kuhakikisha kuwa kama kutakuwa na huduma hii basi
walimu wake waombewe, na watoto waombewe na wazazi waombewe na kwa ujumla
watoto waombewe na wafunguliwe vilevile kama tunavyowasikiliza watu wazima na
kuwaombea
Rev.
Innocent Samuel Kamote
Mkuu
wa wajenzi mwenye Hekima

