Waefeso 4:11-12 “Naye alitoa wengine kuwa
mitume, na wengine kuwa manabii; na wengine kuwa wainjilisti na wengine kuwa
wachungaji na waalimu; kwa kusudi la kuwakamilisha watakatifu, hata kazi ya
huduma itendeke, hata mwili wa Kristo ujengwe;”
Utangulizi:
Ni muhimu kufahamu kuwa kusudi
kubwa la shule ya huduma ndani ya kanisa ni kwaajili ya kukumbushana wajibu
wetu wa kulijenga kanisa la Mungu, Mungu alitoa wengine kuwa Mitume, wengine kuwa
Manabii, wengine kuwa Wainjilisti, wengine kuwa Wachungaji na Walimu kwa kusudi
la kuwakamilisha watakatifu, na kuhakikisha kazi ya huduma inatendeka na mwili
wa Kristo unajengwa kwa hiyo kila mtenda kazi ni mjenzi katika nyumba ya Mungu
Kanisa la Mungu linafananishwa na shamba, linafananishwa na jengo na sisi ndio
wafanyakazi pamoja na Mungu kwa hiyo kila mtenda kazi ni mjenzi katika nyumba
ya Mungu na tunapaswa kuifanya kazi yetu vema na kwa usahihi kwa sababu Mungu
ataipima kazi ya kila mtu kwa hiyo kila mjenzi anapaswa kuwa makini namna
anavyojenga katika jengo la Mungu.
1Wakorintho 3:6-15 “Mimi nilipanda, Apolo
akatia maji; bali mwenye kukuza ni Mungu. Hivyo, apandaye si kitu, wala atiaye
maji, bali Mungu akuzaye. Basi yeye apandaye, na yeye atiaye maji ni wamoja,
lakini kila mtu atapata thawabu yake mwenyewe sawasawa na taabu yake mwenyewe.
Maana sisi tu wafanya kazi pamoja na Mungu; ninyi ni shamba la Mungu, ni jengo
la Mungu. Kwa kadiri ya neema ya Mungu niliyopewa, mimi, kama mkuu wa wajenzi
mwenye hekima, naliuweka msingi, na mtu mwingine anajenga juu yake. Lakini kila
mtu na aangalie jinsi anavyojenga juu yake. Maana msingi mwingine hakuna mtu
awezaye kuuweka, isipokuwa ni ule uliokwisha kuwekwa, yaani, Yesu Kristo.
Lakini kama mtu akijenga juu ya msingi huo, dhahabu au fedha au mawe ya
thamani, au miti au majani au manyasi, kazi ya kila mtu itakuwa dhahiri. Maana siku
ile itaidhihirisha, kwa kuwa yafunuliwa katika moto; na ule moto wenyewe
utaijaribu kazi ya kila mtu, ni ya namna gani. Kazi ya mtu aliyoijenga juu yake
ikikaa, atapata thawabu. Kazi ya mtu ikiteketea, atapata hasara; ila yeye
mwenyewe ataokolewa; lakini ni kama kwa moto.”
Katika nyumba ya Mungu kuna
maeneo mbalimbali ambayo yanatutaka sisi kama watenda kazi kuwa makini, kuwa
macho na kuyasimamia endapo tunataka kanisa letu likue kiroho na liwe kubwa
lenye maelfu ya watu, ikumbukwe kuwa kadiri kanisa linavyokuwa kubwa linahitaji
wahudumu wengi zaidi watakaotoa macho na kuhudumia maeneo mbalimbali na kumbuka
kila tunapohudumu tunahudumia pamoja na Mungu kwa hiyo Baraka za Mungu huwa
kubwa kwa kila mtenda kazi anayeifanya kazi yake kwa uaminifu, watenda kazi
wengi wanapotupia macho maeneo mbalimbali ya kihuduma tunawapa watumishi wa
Mungu nafasi kubwa ya kuomba na kulihudumia neno badala ya kushughulika na
maswala ambayo yangeliweza kuangaliwa na watu wengine, aidha kanisa linapokua
linatakiwa kuwa na wahudumu wengi zaidi ili kuzuia manung’unuiko miongoni mwa
jumuiya ya washirika katika kanisa la
Mungu.
Matendo 6:1-4 “Hata siku zile wanafunzi
walipokuwa wakiongezeka hesabu yao, palikuwa na manung'uniko ya Wayahudi wa
Kiyunani juu ya Waebrania kwa sababu wajane wao walisahauliwa katika huduma ya
kila siku. Wale Thenashara wakawaita jamii ya wanafunzi, wakasema, Haipendezi
sisi kuliacha neno la Mungu na kuhudumu mezani. Basi ndugu, chagueni watu saba
miongoni mwenu, walioshuhudiwa kuwa wema, wenye kujawa na Roho, na hekima, ili
tuwaweke juu ya jambo hili; na sisi tutadumu katika kuomba na kulihudumia lile
Neno.”
Kwa msingi huo basi tutachukua
muda kujifunza somo hili UMUHIMU WA SHULE YA HUDUMA kwa kuzingatia vipengele
vitatu vifuatavyo;-
- Sisi tu wafanyakazi pamoja na Mungu
- Jinsi tunavyoweza kujenga pamoja na
Mungu
- Vema mtumwa mwema na mwaminifu
Sisi tu wafanyakazi pamoja na Mungu.
Paulo mtume anaelezea wazi kuwa
sisi tu wafanyakazi pamoja na Mungu, anasema hayo kwa kusudi la kuweka mkazo
kuwa kazi ya Mungu haiwezi kwenda mbele bila wanadamu, Mungu alimuumba
mwanadamu kwa kusudi la kuwa na ushirika na yeye na kwa sababu hiyo sisi
tunabeba kusudi lote la Mungu hapa duniani, jukumu hili kamwe Mungu hajawahi
kuwapa malaika lakini ametupa sisi, kwa hiyo ni jukumu la kila mtu aliyeokolewa
kulijemga kanisa la Mungu na kuifanya kazi ya Mungu kazi hii iliyo njema.
1Wakorintho 3:9 “Maana sisi tu wafanya kazi
pamoja na Mungu; ninyi ni shamba la Mungu, ni jengo la Mungu.”
2Wakorintho 6:1-2 “Nasi tukitenda kazi
pamoja naye twawasihi msiipokee neema ya Mungu bure. (Kwa maana asema, Wakati
uliokubalika nalikusikia, Siku ya wokovu nalikusaidia; tazama, wakati
uliokubalika ndiyo sasa; tazama siku ya wokovu ni sasa)”
Mungu amempa mwanadamu jukumu zima
la kuihubiri injili na kuieneza na kuwafanya mataifa yote kuwa wanafunzi, hii
ni heshima kubwa sana kwani tunapoifanya kazi hiii Mungu huwa hakuachi anakuwa
pamoja nawe kwa sababu kazi hii sio yetu ni ya kwake kwa hiyo wewe kama mtoto
wake unashirikiana naye katika kuikamilisha hakuna mahali popote ambapo Mungu
alimuagiza mtu kazi kisha akamuacha, wakati wote mtu anapoifanya kazi ya Mungu
neno la Mungu linaonyesha kuwa Bwana akawa pamoja naye
Marko 16:19-20. “Basi Bwana Yesu, baada ya
kusema nao, akachukuliwa juu mbinguni, akaketi mkono wa kuume wa Mungu. Nao
wale wakatoka, wakahubiri kotekote, Bwana akitenda kazi pamoja nao, na
kulithibitisha lile neno kwa ishara zilizofuatana nalo.]”
Paulo anatumia mfano wa shughuli
za kilimo kama kupanda na kumwagilia na hata maswala ya ujenzi kuonyesha kuwa
katika mwili wa Kristo kila mmoja wetu ana majukumu mbalimbali, kutokana na
vipawa mbalimbali na karama mbalimbali
lakini wote sisi tunaifanya kazi moja, kwa hiyo katika shule hii ya
watenda kazi tunaainisha maeneo mbalimbali ya kiutendaji , hata kama wote
tunajifunza hizi ili kumtumikia Mungu kwa pamoja baadae utaweza kuona kuwa
tutamtumikia Mungu sehemu mbalimbali na kufanya huduma mbalimbali lakini katika
mwili huu huu mmoja.
1Wakorintho 12:12-27 “Maana kama vile mwili
ni mmoja, nao una viungo vingi, na viungo vyote vya mwili ule, navyo ni vingi,
ni mwili mmoja; vivyo hivyo na Kristo. Kwa maana katika Roho mmoja sisi sote
tulibatizwa kuwa mwili mmoja, kwamba tu Wayahudi, au kwamba tu Wayunani; ikiwa
tu watumwa au ikiwa tu huru; nasi sote tulinyweshwa Roho mmoja. Kwa maana mwili
si kiungo kimoja, bali ni vingi. Mguu ukisema, Kwa kuwa mimi si mkono, mimi si
wa mwili; je! Si wa mwili kwa sababu hiyo? Na sikio likisema, Kwa kuwa mimi si
jicho, mimi si la mwili; je! Si la mwili kwa sababu hiyo? Kama mwili wote ukiwa
jicho, ku wapi kusikia? Kama wote ni sikio ku wapi kunusa? Bali Mungu amevitia
viungo kila kimoja katika mwili kama alivyotaka. Lakini kama vyote vingekuwa
kiungo kimoja, mwili ungekuwa wapi? Lakini sasa viungo ni vingi, ila mwili ni
mmoja. Na jicho haliwezi kuuambia mkono, Sina haja na wewe; wala tena kichwa
hakiwezi kuiambia miguu, Sina haja na ninyi. Bali zaidi sana vile viungo vya
mwili vidhaniwavyo kuwa vinyonge zaidi vyahitajiwa zaidi. Na vile viungo vya
mwili vidhaniwavyo kuwa havina heshima, viungo vile twavipa heshima zaidi; na
viungo vyetu visivyo na uzuri vina uzuri zaidi sana. Kwa maana viungo vyetu
vilivyo na uzuri havina uhitaji; bali Mungu ameuungamanisha mwili, na kukipa
heshima zaidi kile kiungo kilichopungukiwa;ili kusiwe na faraka katika mwili,
bali viungo vitunzane kila kiungo na mwenziwe. Na kiungo kimoja kikiumia,
viungo vyote huumia nacho, na kiungo kimoja kikitukuzwa, viungo vyote hufurahi
pamoja nacho. Basi ninyi mmekuwa mwili wa Kristo, na viungo kila kimoja peke
yake.”
Kwa hiyo tutafanya kazi katika
maeneo tofauti tofauti wakati mwingine kwa kupangiwa au wakati mwingine
kutokana na kile kitu ambacho Mungu amekiweka ndani yako lakini sisi sote tu
watenda kazi na tufahamu kuwa tunaifanya kazi moja, asitokee mtenda kazi akafikiri
kuwa hajaheshimiwa kwa kupangiwa eneo fulani, kokote tutakakoenda kumbuka Bwana
yuko pamoja nawe na anajua kuwa unaujenga mwili wa Kristo, aidha tunafanya
huduma hizi kwa neema ya Mungu kwa hiyo neema zinatofautiana kinachotakiwa
kwetu ni uaminifu, usitake kuwa na huduma kama ya fulani kwa sababu kila mmoja
ana neema tofauti na hivyo tutatumia neema hizo kwa kufaidiana
Waefeso 4:7-8 “Lakini kila mmoja wetu
alipewa neema kwa kadiri ya kipimo cha kipawa chake Kristo. Hivyo husema,
Alipopaa juu aliteka mateka, Akawapa wanadamu vipawa.”
1Petro 10-11 “kila mmoja kwa kadiri
alivyoipokea karama, itumieni kwa kuhudumiana; kama mawakili wema wa neema
mbalimbali za Mungu. Mtu akisema, na aseme kama mausia ya Mungu; mtu akihudumu,
na ahudumu kwa nguvu anazojaliwa na Mungu; ili Mungu atukuzwe katika mambo yote
kwa Yesu Kristo. Utukufu na uweza una yeye hata milele na milele. Amina.”
Warumi 12:3-5 “Kwa maana kwa neema
niliyopewa namwambia kila mtu aliyeko kwenu asinie makuu kupita ilivyompasa
kunia; bali awe na nia ya kiasi, kama Mungu alivyomgawia kila mtu kiasi cha
imani. Kwa kuwa kama vile katika mwili mmoja tuna viungo vingi, wala viungo
vyote havitendi kazi moja; Vivyo hivyo na sisi tulio wengi tu mwili mmoja katika
Kristo, na viungo, kila mmoja kwa mwenzake.”
Kwa hiyo utaweza kuona Mungu
ametuita kutenda kazi pamoja naye kwa neema na vipawa na karama tofauti
tofauti, tutumie kila alichotupa Mungu kumtumikia bila kuumiza mwili wa Kristo
kwa migawanyiko na manung’uniko mbalimbali kwani wote tutaifanya kazi hii kwa
kufikia lengo moja kuufikia ulimwengu na kuwaleta watu kwa Yesu na kulijenga
kanisa lake ili baada ya utumishi wetu duniani tukakae naye kule mbinguni
Jinsi tunavyoweza kujenga pamoja na Mungu
Katika kanisa la Mungu kuna namna
mbalimbali za utumishi ambazo kwazo tunaweza kuzitumia katika kumtumikia Mungu,
Ni muhimu kwetu kufahamu kuwa tukiifanya kazi hii ya Mungu kwa hiyari, kwa moyo
na kwa uaminifu Mungu mwenyewe atakupa thawabu na kukupongeza na kukufuta machozi
kwa kazi hii ambayo ina upinzani kutoka kwa adui shetani lakini simama kwa
uaminifu kwaajili ya Bwana kama alivyofanya mtume Paulo ambaye alivumilia
Mathayo 25:21-23. “Akaja yule aliyepokea
talanta tano, akaleta talanta nyingine tano, akisema, Bwana, uliweka kwangu
talanta tano; tazama, talanta nyingine tano nilizopata faida. Bwana wake
akamwambia, Vema, mtumwa mwema na mwaminifu; ulikuwa mwaminifu kwa machache,
nitakuweka juu ya mengi; ingia katika furaha ya bwana wako. Akaja na yule
aliyepokea talanta mbili, akasema, Bwana, uliweka kwangu talanta mbili; tazama,
talanta nyingine mbili nilizopata faida. Bwana wake akamwambia, Vema, mtumwa
mwema na mwaminifu; ulikuwa mwaminifu kwa machache, nitakuweka juu ya mengi;
ingia katika furaha ya bwana wako.”
Washirika wanapohudumiwa vema na
kufikiwa katika mazingira yote hasa katika makanisa makubwa wanaona kuwa
wanajaliwa hata kama hawamuoni mchungaji kiongozi kutokana na majukumu yake
umoja wa kanisa utaimarika, kanisa letu litakuwa kwa kasi kwa ukuaji wa aina
zote nazungumzia ukuaji wa kiroho, ukomavu na wa kiidadi na kuwa kanisa la
maelfu, umoja utaimarika hata pamoja na ukubwa wa kanisa, na wingi wetu
utageuka utajiri na afya ya kila mmoja wetu na miujiza haitakoma umati utavuta
umati na Mungu atataka kujidhihirisha kwenye kusanyiko la watu wengi, sasa haya
ndio maeneo na mazingira tunayoweza kumtumikia Mungu wetu:-
- Kuwahudumiwa waamini wapya –
Mojawapo ya eneo Muhimu sana ambalo watenda kazi wote, wanafunzi wote na
wenye hekima wote tunapaswa kulipa uzito mkubwa sana sana ili tupate
kanisa lililobora ni kuwahudumia waamini wapya, au kuwahudumia watoto
wachanga kiroho, kuwafuatilia, kuwalisha kwa neno la Mungu na kufanya
malezi, Kama tunampenda sana Yesu upendo wetu utaonekana kwa jinsi
tunavyowalisha kondoo zake
Yohana 21:15-17 “Basi walipokwisha kula, Yesu akamwambia Simoni Petro, Je!
Simoni wa Yohana, wewe wanipenda kuliko hawa? Akamwambia, Naam, Bwana, wewe
wajua kuwa nakupenda. Akamwambia, Lisha wana-kondoo wangu. Akamwambia tena mara
ya pili, Simoni wa Yohana, wanipenda? Akamwambia, Ndiyo, Bwana, wewe wajua kuwa
nakupenda. Akamwambia, Chunga kondoo zangu. Akamwambia mara ya tatu, Simoni wa
Yohana, wanipenda? Petro alihuzunika kwa vile alivyomwambia mara ya tatu,
Wanipenda? Akamwambia, Bwana, wewe wajua yote; wewe umetambua ya kuwa
nakupenda. Yesu akamwambia, Lisha kondoo zangu.”
Agizo hili ni pana kwani linahusu ulishaji mzima wa kondoo,
watumishi wa Mungu walioitwa katika wito maalumu wataifanya kazi ya kuwalisha
kondoo katika ibada, tulizojipangia na katika semina zitakazojitokeza na
kadhalika, lakini watenda kazi, wanafunzi na wenye hekima (Wiseman) wao
watapaswa kuhakikisha kuwa wanawahudumia na kuwalisha watoto wachanga kiroho
kwa kuwafundisha masomo ya mwanzo ya wokovu, ukiwaimarisha waamini wapya katika
wokovu, kwa kuwaombea, kwa kuwafundisha kuisoma Biblia, na kuwaelekeza kuhusu
maisha tamaduni na Misingi ya imani ya kanisa letu
- Kuwahudumia waamini wote ibadani - Eneo lingine la huduma zetu kama
watendakazi, wanafunzi na wenye hekima ni kuwahudumia watu wote
wanaohudhuria ibada katika kanisa letu, watu waliopitia shule hii ya
huduma watawahudumia watu kwa kuwapokea vizuri na kwa heshima, kuwapokelea
vitu vyao, watoto na kuwaongoza mahali sahihi pa kuketi, sio hivyo tu kama
ni mgeni utafanya kila jitihada kutambua anaitwa nani namba zake za simu
na atakuwa pamoja nasi kwa muda gani, kama ni wadhaifu tutawatia nguvu, na
tutaanza kuwapandisha imani kuwa umefanya uamuzi wa busara kuja kuabudu
katika kanisa letu hili zuri, hakikisha kuwa kila mtu ana mazingira salama
ya kuabudu, atajua vyoo viko wapi, wasaidie kujua mambo muhimu wanayopaswa
kuyajua, tutakuwa tayari kuhudumu pamoja na Muhubiri katika ibada kuu na
maombezi na kusawaidia watu wanaoanguka kwa mapepo au nguvu za Mungu na
wale wanaofunguliwa na kuhakikisha kuwa tunawahifadhi kwa nguo maalumu
safi na kuwafunika, Pia kuwapeleka mahali salama na sahihi zaidi na katika
ibada nyingine maalumu kama ubatizo, meza ya Bwana, kubariki watoto, na
kadhalika
Yohana 10:14 “Mimi ndimi mchungaji mwema; nao walio wangu nawajua; nao
walio wangu wanijua mimi”
1Wathesalonike 5:14
“Ndugu, twawasihi, waonyeni wale wasiokaa kwa
utaratibu; watieni moyo walio dhaifu; watieni nguvu wanyonge; vumilieni na watu
wote.”
Waefeso 4:1-3 “Kwa hiyo nawasihi, mimi niliye mfungwa katika Bwana,
mwenende kama inavyoustahili wito wenu mlioitiwa; kwa unyenyekevu wote na
upole, kwa uvumilivu, mkichukuliana katika upendo; na kujitahidi kuuhifadhi
umoja wa Roho katika kifungo cha amani.”
- Kusaidia huduma ya kichungaji – Watendakazi
wote, wanafunzi na wenye hekima wanapaswa pia kufanya kazi ya kutoa msaada
wa huduma ya kichungaji, ikumbukwe kuwa Mchungaji hawezi kufanya kila kitu
peke yake, na akilazimika kufanya yote muda wa kukaa katika neno la Mungu
na maombi utafilisiwa na kuathiri huduma za kiroho za jumla na ndio maana mitume waliona vema kuwa
na mashemasi kwaajili ya majukumu
Matendo 6:1-7 “Hata siku zile wanafunzi walipokuwa wakiongezeka hesabu
yao, palikuwa na manung'uniko ya Wayahudi wa Kiyunani juu ya Waebrania kwa
sababu wajane wao walisahauliwa katika huduma ya kila siku. Wale Thenashara
wakawaita jamii ya wanafunzi, wakasema, Haipendezi sisi kuliacha neno la Mungu
na kuhudumu mezani. Basi ndugu, chagueni watu saba miongoni mwenu,
walioshuhudiwa kuwa wema, wenye kujawa na Roho, na hekima, ili tuwaweke juu ya
jambo hili; na sisi tutadumu katika kuomba na kulihudumia lile Neno. Neno hili
likapendeza machoni pa mkutano wote; wakamchagua Stefano, mtu aliyejaa imani na
Roho Mtakatifu, na Filipo, na Prokoro, na Nikanori, na Timoni, na Parmena, na
Nikolao mwongofu wa Antiokia; ambao wakawaweka mbele ya mitume, na walipokwisha
kuomba wakaweka mikono yao juu yao. Neno la Mungu likaenea; na hesabu ya wanafunzi
ikazidi sana katika Yerusalemu; jamii kubwa ya makuhani wakaitii ile Imani.”
Warumi 16:3-4. “Nisalimieni Priska na Akila, watenda kazi pamoja nami
katika Kristo Yesu; waliokuwa tayari hata kukatwa kichwa kwa ajili ya maisha
yangu; ambao ninawashukuru, wala si mimi tu, ila na makanisa ya Mataifa yote
pia; nisalimieni na kanisa lililomo katika nyumba yao.”
Kutoka 18:17-22 “Mkwewe Musa akamwambia, Jambo hili ufanyalo si jema. Huna
budi utadhoofika wewe, na hawa watu walio pamoja nawe pia; maana jambo hili ni
zito mno kwako; huwezi wewe kulitenda peke yako. Sikiza sasa neno langu,
nitakupa shauri, na Mungu na awe pamoja nawe; uwe wewe kwa ajili ya watu mbele
ya Mungu, nawe umletee Mungu maneno yao; nawe utawafundisha zile amri na
sheria, nawe utawaonyesha njia ambayo inawapasa kuiendea, na kazi ambayo
inawapasa kuifanya. Zaidi ya hayo utajipatia katika watu hawa watu walio na
uwezo, wenye kumcha Mungu, watu wa kweli, wenye kuchukia mapato ya udhalimu;
ukawaweka juu yao, wawe wakuu wa maelfu, na wakuu wa mia, na wakuu wa hamsini,
na wakuu wa kumi; nao wawaamue watu hawa sikuzote; kisha, kila neno lililo
kubwa watakuletea wewe, lakini kila neno dogo wataliamua wenyewe; basi kwako
wewe mwenyewe utapata nafasi zaidi, nao watauchukua huo mzigo pamoja nawe.”
Wasaidizi wa huduma ya kichungaji watafanya majukumu ambayo
yangewezwa kufanywa na mchungaji katika kanisa, majukumu hayo ni pamoja na
kuwatembelea washirika, kuwasaidia katika maombi, kufanya ufuatiliaji, na
kufanya uashauri wa kichungaji, huduma hizi zote zinafanyika chini ya utumishi
wa mchungaji kiongozi katika kanisa
- Kuwahudumia wale wanaotokwa na pepo
– watenda kazi, wanafunzi na wenye hekima ni wajibu wao kuhakikisha kuwa
mambo yote katika nyumba ya Bwana yanafanyika kwa kufuata utaratibu, Mungu
ni Mungu wa utaratibu na anataka mambo yote yafanyike kwa utaratibu, kwa
msingi huo, moja ya huduma wanayotakiwa kuifanya ni kuwahudumia wenye
kuteswa na mapepo hasa katika ibada za maombezi, wanaousumbuliwa na pepo
kama ni wakati ibada inaendelea ni lazima wahamishiwe kwenye vyumba
maalumu vya maombezi, lakini kama machungaji yuko katika kuwashughulikia
na wanaangushwa au kusumbua miongoni mwa watu watolewe na kupelekwa mbele
au sehemu maalumu wanakoweza kuwa na nafasi ya kuhudumiwa na kufunguliwa
kanisa linapokuwa tayari na watendakazi wanapokuwa tayari kuhudumu pamoja
na Mchungaji na kuhudumu pamoja na Roho wa Mungu kwa utaratibu maalumu,
Mungu Roho Mtakatifu atafanya miujiza mikubwa zaidi, kama pepo watasumbua
wakati neno la Mungu linaendelea, wenye pepo wapelekwe sehemu nyingine ili
neno la Mungu lihubiriwe kwanza, na wasipoteze usikivu!
1Wakorintho 14:39-40
“Kwa ajili ya hayo, ndugu, takeni sana kuhutubu,
wala msizuie kunena kwa lugha. Lakini mambo yote na yatendeke kwa uzuri na kwa
utaratibu.”
Waefeso 6:11-12 “Vaeni silaha zote za Mungu, mpate kuweza kuzipinga hila
za Shetani. Kwa maana kushindana kwetu sisi si juu ya damu na nyama; bali ni
juu ya falme na mamlaka, juu ya wakuu wa giza hili, juu ya majeshi ya pepo
wabaya katika ulimwengu wa roho.”
Mapepo yanaweza kuwaathiri watu lakini kumbuka kuwa watu
sio pepo, kwa hiyo utu wa aliyeathiriwa uthaminiwe na atunzwe kwa heshima zote,
tusiwakasirikie wala tusiwe na msisimko ni lazima tuwe wapole na waungwana
tuwahifadhi tuwasaidie kufunguka, tuwapeleke sehemu maalumu zilizoainishwa,
tuwafute vizuri na tuchukue taarifa zao kwaajili ya ufuatiliaji na kwaajili ya
kutunza muujiza na ushuhuda wa baadae
Mwondoe mwemye pepo katikati ya umati wa watu, kama
ikiwezekana, tumia mamlaka kwa ustaarabu kuyakemea na sio kelele, usitumie nguvu
kumbuka pepo wanatoka kwa jina la Yesu na kwa nguvu za Roho Mtakatifu wewe na
mimi sio tunaotoa pepo, Pepo wanatolewa na Roho, sisi wajibu wetu ni kuwapa
imani na kuwasaidia wao kupokea muujiza wao, msikemee watu wengi pepo mmoja
mamlaka moja inatosha.
Mathayo 12:28-29 “Lakini mimi nikitoa pepo kwa Roho wa Mungu, basi ufalme
wa Mungu umekwisha kuwajilia. Ama awezaje mtu kuingia ndani ya nyumba ya mtu
mwenye nguvu na kuviteka vyombo vyake, asipomfunga kwanza yule mwenye nguvu?
Ndipo atakapoiteka nyumba yake.”
2Timotheo 2:24 “Tena haimpasi mtumwa wa Bwana kuwa mgomvi; bali kuwa
mwanana kwa watu wote, awezaye kufundisha, mvumilivu;”
- Kuwahudumia watu wanaoangushwa chini –
uwe na uwezo wa kutambua ni aina gani ya sababu imempeleka mtu chini,
sio kila anayeanguka chini ni kwa sababu ya pepo, wengine wanaweza kuigiza
tu, na wengine wanaweza kuwa wamehemewa na hisia kali, na wengine ni kwa
sababu ya nguvu za Mungu anaangushwa chini lakini anaweza asiwe na pepo,
kwa hiyo usikimbilie kukemea pepo, kwa sababu wengine huangushwa tu na
nguvu za Mungu na anaweza kujisikia vibaya kudhaniwa kuwa ana pepo.
Luka 5:16-17 “Lakini yeye alikuwa akijiepua, akaenda mahali pasipokuwa
na watu, akaomba.Ikawa siku zile mojawapo alikuwa akifundisha, na Mafarisayo na
waalimu wa torati walikuwa wameketi hapo, waliotoka katika kila kijiji cha
Galilaya, na Uyahudi, na Yerusalemu; na uweza wa Bwana ulikuwapo apate kuponya.”
Ufunuo 1:17-18 “Nami nilipomwona, nalianguka miguuni pake kama mtu
aliyekufa. Akaweka mkono wake wa kuume juu yangu, akisema, Usiogope, Mimi ni wa
kwanza na wa mwisho, na aliye hai; nami nalikuwa nimekufa, na tazama, ni hai
hata milele na milele. Nami ninazo funguo za mauti, na za kuzimu.”
Wahudumu, watendakazi, wanafunzi na wenye hekima kumbuka ya
kuwa lolote linaweza kutokea wakati wa maombezi, na wakati wa ibada jiandae
kusimama nyuma kwa huduma, kwa wale wanaohudumiwa, jiepushe kusukuma watu, tunza heshima ya watu
hususani wanawake, wafunike wanapokuwa wamekaa vibaya, hakikisha kunakuwa na
utulivu na amani tengeneza mazingira ya Amani, wasaidie kwa upole, omba kimya
kimya, na usiwakasirikie wala kuwaudhi wao ni kama wagonjwa wetu na sisi ndio
wahudumu wao, jua ya kuwa Mungu ndiye anayewahudumia pamoja nawe kwa sababu
hiyo tuwahudumie kwa huruma na upendo
- Kuwahudumia wageni ambao ni mara yao
ya kwanza – Wakristo wanahimizwa kuwa wakarimu, unapowapokea watu
vizuri kwa tabasamu la upendo na kuwapa muongozo mzuri, bila papara na kwa
kuwaonyesha upendo wao watajua kuwa kweli hapa ni kanisani, kanisani ni
mahali ambapo watu wanapaswa kupokelewa kwa upendo kuliko mahali kokote
kule, kanisani ni zaidi ya dukani, hotelini, gengeni na kadhalika waonyeshe watu uungwana
mkubwa, msalimie vizuri, mpe ratiba na muelekeo wa ibada, usimuache akajitenga, zungumza kwa lugha
za kawaida, waonyeshe shukurani waonyeshe kuwafuatailia baada ya ibada,
wageni wangependa kuagana na mtu yule yule aliyempokea mwanzoni hasa kama
ulimpokea vizuri, kwa hiyo yule utakayempokea mwanzoni ni mteja wako mpaka
mwisho usimpoteze
Waebrania 13:1-2 “Upendano wa ndugu na udumu. Msisahau kuwafadhili wageni;
maana kwa njia hii wengine wamewakaribisha malaika pasipo kujua.”
Yohana 13:34-35 “Amri mpya nawapa, Mpendane. Kama vile nilivyowapenda
ninyi, nanyi mpendane vivyo hivyo. Hivyo watu wote watatambua ya kuwa ninyi
mmekuwa wanafunzi wangu, mkiwa na upendo ninyi kwa ninyi.”
1Wakorintho 9:19-23
“Maana, ingawa nimekuwa huru kwa watu wote,
nalijifanya mtumwa wa wote, ili nipate watu wengi zaidi. Nalikuwa kama Myahudi
kwa Wayahudi, ili niwapate Wayahudi; kwa wale walio chini ya sheria, nalikuwa
kama chini ya sheria, (ingawa mimi mwenyewe si chini ya sheria), ili niwapate
walio chini ya sheria. Kwa wale wasio na sheria nalikuwa kama sina sheria, (si
kwamba sina sheria mbele za Mungu, bali mwenye sheria mbele za Kristo), ili
niwapate hao wasio na sheria. Kwa wanyonge nalikuwa mnyonge, ili niwapate
wanyonge. Nimekuwa hali zote kwa watu wote, ili kwa njia zote nipate kuwaokoa
watu. Nami nafanya mambo yote kwa ajili ya Injili ili kuishiriki pamoja na
wengine.”
- Kuwahudumia viongozi wa serikali – Viongozi
wa serikali na viongozi wakubwa wa kitaifa wanaweza kuwa wakristo wenzetu
katika kanisa la Mungu lakini pia wanaweza kuwa rafiki zetu na wanaweza
kutembelea kanisa letu kwa taarifa au ghafla watendakazi katika kanisa
tunapaswa kuwahudumia kwa heshima na ustaarabu pia, heshimu nafasi waliyo
nayo lakini usiwaabudu, usilichuje neno la Mungu kwaajili yao, weka heshima
sawa na maelekezo ya injili, Mungu
hana upendeleo, lakini anayestahili heshima heshima, viongozi wahudumiwe
vizuri na kukaribishwa na kama iko sehemu maalumu ya wageni maalumu
wanaweza kuelekezwa hapo, kama ni kiongozi mwenye itifaki (Protocol) kadhaa wasikilize
viongozi wa itifaki walioambatana naye na shirikiana nao katika utaratibu
mzuri, mawasiliano mazuri na kadhalika, kauli za kisiasa kanisani
haziruhusiwi, unabii unaohusu wanasiasa, haufai, isipokuwa kama Mungu
amesema hivyo, na hakuna sababu za kulazimisha maombi ya kitaifa kama
hakukuwa na programu hiyo msibadili gea angani, jiamini, tunza heshima
jiepushe na mizaha inayoweza kutafasiriwa vibaya maneno yako yajae neema.
Warumi 13:7-8 “Wapeni wote haki zao; mtu wa kodi, kodi; mtu wa ushuru,
ushuru; astahiliye hofu, hofu; astahiliye heshima, heshima. Msiwiwe na mtu cho
chote, isipokuwa kupendana; kwa maana ampendaye mwenzake ameitimiza sheria.”
1Petro 2:17 “Waheshimuni watu wote. Wapendeni ndugu. Mcheni Mungu.
Mpeni heshima mfalme”
Wakolosai 4:5-6. “Enendeni kwa hekima mbele yao walio nje, mkiukomboa
wakati. Maneno yenu yawe na neema siku zote, yakikolea munyu, mpate kujua jinsi
iwapasavyo kumjibu kila mtu.”
- Kuwahudumia watumishi wa Mungu – Watenda
kazi, wahudumu, wanafunzi pamoja na wenye hekima katika kanisa wanawajibu
pia wa kumuhudumia mchungaji, wakati wote huduma inapoendelea pamoja na
shughuli nyingine tutakuwa katika maombi ya kimya kimya tukiendelea
kuhudumu pamoja na mtumishi wa Mungu, wafunikwe kwa kuwaombea, uwe na
karama ya kupambanua roho na kung’amua kwa haraka watu wanaotaka kuwashambulia
watumishi wa Mungu, angalia kama amechoka, angalia kama amekata tamaa,
angalia kama anapingwa, angalia kama anahitaji kitambaa cha jasho, maji ya
kunywa ama kama analetewa kitu kibaya, wekeni utaratibu wa ulinzi na
usalama kwaajili ya kanisa zima na kwaajili ya mtumishi wa Mungu, dhibiti
watu kumfikia kwa haraka bila utaratibu, au wale wanaotaka kumshambulia, wekeni
timu ya itifaki ya namna ya kumfikia mtumishi wa Mungu, kataza
wanaomsengenya, wasahihishe wasiomuelewa, mlinde bila kupigana, muheshimu
bila kumuabudu, heshimu mipaka, wajibika kwake, lindeni kile Mungu ameweka
ndani yake, Mke wake na familia yake na kadhalika, tunapowahudumia watumishi wa
Mungu tunamuhudumia Mungu pia.
Yohana 12:20-21. “Palikuwa na Wayunani kadha wa kadha miongoni mwa watu
waliokwea kwenda kuabudu kwenye sikukuu. Basi hao walimwendea Filipo, mtu wa
Bethsaida ya Galilaya, wakamwomba, wakisema, Bwana, sisi tunataka kumwona Yesu.
Filipo akaenda, akamwambia Andrea; kisha Andrea na Filipo wakamwambia Yesu.”
Zaburi 105:14-15”Hakumwacha mtu awaonee, Hata wafalme aliwakemea kwa ajili
yao. Akisema, Msiwaguse masihi wangu, Wala msiwadhuru nabii zangu.”
1Timotheo 5:17 “Wazee watawalao vema na wahesabiwe kustahili heshima
maradufu; hasa wao wajitaabishao kwa kuhutubu na kufundisha”
Na. Rev. Innocent Samuel Kamote
Mkuu wa wajenzi mwenye Hekima


