Jumapili, 12 Aprili 2026

Kuyachuchumilia yaliyo mbele!

 


Wafilipi 3:12-14 “Si kwamba nimekwisha kufika, au nimekwisha kuwa mkamilifu; la! Bali nakaza mwendo ili nipate kulishika lile ambalo kwa ajili yake nimeshikwa na Kristo Yesu. Ndugu, sijidhanii nafsi yangu kwamba nimekwisha kushika; ila natenda neno moja tu; nikiyasahau yaliyo nyuma, nikiyachuchumilia yaliyo mbele; nakaza mwendo, niifikilie mede ya thawabu ya mwito mkuu wa Mungu katika Kristo Yesu.”



Utangulizi:

Mojawapo ya changamoto kubwa sana katika ufanisi wa maendeleo ya mwanadamu kiroho na kimwili na kisaikolojia ni pamoja na kutokusahau yaliyo nyuma, “Living in the Past” kutokuyasahau yaliyo nyuma kumewafunga watu wengi sana na kuwawekea mipaka ya kiimani, kuchelewesha ukuaji wao wa kiroho, kuzuia maendeleo yao ya safari ya kiuchumi, kuwadumaza katika hali zote kuwanyima maisha ya ushindi, kuathiri uwezo wa kufanya maamuzi, kupunguza nguvu zao kwa mambo yajayo na kushindwa kuamini ahadi ya Mungu kuhusu mambo yajayo, hali hii iliwasumbua sana wana wa Israel ambao hata walipookolewa kutoka Misri, hawakuliona baadaye tendo lile kuwa ni kubwa sana na badala yake walinung’unika mara kwa mara wakikumbuka kule Mungu alikowaokoa katika inchi ya utumwa, tena wakikumbuka vitu vidogovidogo kama matango na mboga.

Hesabu 11:4-6 “Kisha mkutano wa wafuasi waliokuwa kati yao, wakashikwa na tamaa; wana wa Israeli nao wakalia tena, wakasema, N'nani atakayetupa nyama tule? Twakumbuka samaki tuliokula huko Misri bure; na yale matango, na matikiti, na mboga, na vitunguu, na vitunguu saumu; lakini sasa roho zetu zimekauka; hapana kitu cho chote; hatuna kitu cha kutumaini isipokuwa hii mana tu.”

Kutokuyasahau yaliyo nyuma na kuamua kuyachuchumilia yaliyo mbele kunaweza kukufanya usizione sababu za wito wa Mungu na baraka alizokusudia kwako, kumbuka kila kitu duniani kina mchakato na maisha yana mchakato wake na mwandishi wa mchakato huo ni Mungu, sasa basi anapokuwa amekupitisha mahali na ukawa unalalamika unaweza kusababisha kupoteza Baraka zilizokusudiwa kwako, kwa msingi huo basi leo tutachukua muda kujifunza somo hili muhimu “Kuyachuchumilia yaliyo mbele” kwa kuzingatia vipengele vikuu muhimu vitatu vifuatavyo:-

·         Maana ya kuyachuchumilia yaliyo mbele

·         Umuhimu wa Kuyachuchumilia yaliyo mbele!

·         Athari za kutoyasahau yaliyo nyuma


Maana ya kuyachuchumilia yaliyo mbele

Wafilipi 3:13 “Ndugu, sijidhanii nafsi yangu kwamba nimekwisha kushika; ila natenda neno moja tu; nikiyasahau yaliyo nyuma, nikiyachuchumilia yaliyo mbele;”

Kabla hatujaingia ndani kuangalia kile ambacho Mungu amekusudia kusema nasi leo ni muhimu kwetu kuyafanyia uchunguzi maandiko au maneno yanayotumiwa na Paulo Mtume katika fungu hili la maandiko yana maana gani, Waraka huu wa wafilipi uliandikwa kwa lugha ya kiyunani (Koine Greek) ambayo ndiyo ilikuwa lugha ya kisomi na kitaaluma ya nyakati za karne ya kwanza kwa hiyo kitabu hiki kiliandikwa mnamo mwaka wa 62BK  na maneno haya kuyachuchumilia yaliyo mbele yanasomeka hivi katika kiyunani (Epekteinomenos tois emprosthen)  neno Epekteinomenos au epekteinomai kwa kiingereza linasomeka “stretching oneself forward“ ambalo maana yake ni kujinyoosha kuelekea mbele kwa nguvu  neno hili hasa lina asili ya mkao anaotakiwa kujiweka mwanariadha anapokimbia mbio za Olympic  ili aweze kushinda, kulingana na sheria za Olympic umaliziaji wa mkimbiaji wa riadha huamuliwa wakati kiwiliwili chake kinapovuka mstari wa kumalizia, kwa hiyo katika mbio za riadha kutanguliza miguu au mikono hakuhesabiwi kama umaliziaji wa mbio ulio halali, aidha mwanariadha anayetafuta ushindi huwaga hana muda wa kuangalia nyuma wala pembeni nguvu zake zote  fahamu zake zote huelekezwa katika kufikia lengo na kwa sababu hiyo kila msuli na kila mfumo wa fahamu na neva hufanya kazi kwa bidii kuelekea katika malengo yake, Kwa hiyo Paulo mtume anatumia mfano wa wanariadha kwa sababu ilikuwa maarufu sana nyakati za kanisa la kwanza, wakati wote Mungu anapotaka ushindi utokee katika maisha ya watu wake huwaambia wasonge mbele

Isaya 43:18-19 “Msiyakumbuke mambo ya kwanza, wala msiyatafakari mambo ya zamani.Tazama, nitatenda neno jipya; sasa litachipuka; je! Hamtalijua sasa? Nitafanya njia hata jangwani, na mito ya maji nyikani.”

Kutoka 14:14-15. “BWANA atawapigania ninyi, nanyi mtanyamaza kimya. BWANA akamwambia Musa, Mbona unanililia mimi? Waambie wana wa Israeli waendelee mbele.”  

Unaona! Katika fundisho lake Paulo Mtume hataki Wafilipi wajidhanie kuwa wamekwisha kufika au wamekuwa wakamilifu akitumia mfano wake anamtaka kila Mkristo kusonga mbele kwa nguvu kwa imani na utii, kwa bidii, kwa nguvu kwa tumaini na kutokuangalia nyuma mpaka kuhakikisha ya kuwa tunapata tuzo mbinguni na kuyafikia malengo yetu yaliyo mbele, kwa hiyo kama mwanariadha uliye katika mbio za ushindani wa kiroho angalia mbele tu!

Umuhimu wa Kuyachuchumilia yaliyo mbele!

Ni muhimu kujiuliza kwa nini Paulo Mtume siku zote alikuwa akiyachuchumilia yaliyo mbele na akisahau yaliyo nyuma, Kuangalia nyuma kungempa historia ya matukio yaliyopita ambayo kimsingi yangemshika na kumpunguzia mwendo wake wa kusonga mbele katika imani aku kumpa kuridhika sawa na mwanariadha anavyoweza kupoteza mwelekeo kama ataangalia nyuma, Yeye alikuwa mtu mwenye bidii katika Torati kuliko mtu yeyote, aliishika sheria kiasi ambacho kwa habari ya sheria hakuwa na dhambi, lakini alipompata Yesu na kubaini ubora wa Yesu Kristo hata pamoja na mateso makali yaliyokuwa yakimpata alidhamiria kuwa ataendelea kuwa na Yesu, hatamuacha Yesu atashikamana na Yesu atashikamana na injili na hatarudi nyuma kwa sababu yoyote, aliwaonya Wafilipi hivi na kujionyesha yeye mwenyewe kuwa mfano kwa sababu ya watu waliofundisha mafundisho ya Sheria ya Musa na tohara ambao yeye aliwaitwa umbwa au watu wajikatao akitaka kuwaonyesha Wafilipi faida ya kumfuata Yesu na kuachana na mafundisho ya kale yasiyo na msingi, Paulo alikuwa na mafanikio makubwa katika dini ya kiyahudi na heshima kubwa lakini alipuuzia kwaajili ya Kristo. Alipompata Kirsto hakuangalia pembeni tena alikaza kwenda mbele

Yeye aliliudhi Kanisa 1Wakorintho 15:9 “Maana mimi ni mdogo katika mitume, nisiyestahili kuitwa mitume, kwa sababu naliliudhi Kanisa la Mungu.”

Wagalatia 1:13-15 “Maana mmesikia habari za mwenendo wangu zamani katika dini ya Kiyahudi, kwamba naliliudhi kanisa la Mungu kupita kiasi, nikaliharibu. Nami naliendelea katika dini ya Kiyahudi kuliko wengi walio hirimu zangu katika kabila yangu, nikajitahidi sana katika kuyashika mapokeo ya baba zangu. Lakini Mungu, aliyenitenga tangu tumboni mwa mama yangu, akaniita kwa neema yake,”

Wafilipi 3:2-7 “Jihadharini na mbwa, jihadharini na watendao mabaya, jihadharini na wajikatao. Maana sisi tu tohara, tumwabuduo Mungu kwa Roho, na kuona fahari juu ya Kristo Yesu, wala hatuutumainii mwili.Walakini mimi ningeweza kuutumainia mwili. Mtu ye yote akijiona kuwa anayo sababu ya kuutumainia mwili, mimi zaidi. Nalitahiriwa siku ya nane, ni mtu wa taifa la Israeli, wa kabila ya Benyamini, Mwebrania wa Waebrania, kwa habari ya kuishika torati, ni Farisayo, kwa habari ya juhudi, mwenye kuliudhi Kanisa, kwa habari ya haki ipatikanayo kwa sheria sikuwa na hatia. Lakini mambo yale yaliyokuwa faida kwangu, naliyahesabu kuwa hasara kwa ajili ya Kristo.”

Kila mtu aliyemuamini Bwana wetu Yesu Kristo kama Bwana na mwokozi wa maisha yake anapaswa kusahau yote yaliyopita na kuweka akili zake zote na nguvu zake zote na moyo wake wote na fahamu zake zote kuyachuchumilia yaliyo mbele, hii haimaanishi kuyafuta kabisa lakini maana yake maisha yaliyopita kama yalikuwa ya raha au ya taabu yalikuwa ya heshima ama kuvunjiwa heshima, yasiwe na machango wowote katika hali yako ya sasa kwa kukufanya kuangalia nyuma na kumpuuzia Kristo na badala yake kujitoa kwa nguvu zetu zote katika kumcha Mungu na kumtumikia bila hata kujali hali unayopitia sasa, Neno la Mungu linaonyesha wazi kuwa Mungu havuitiwi kamwe na watu wasio na maamuzi thabiti na badala yake anawataka watu wenye msimamo watakaosonga mbele wazima wazima na sio nusu nusu, ushindi wetu utapatikana sio kwa kuitanguliza mguu au mkono bali kiwiliwili chote

-Mke wa Lutu alitazama nyuma wakati Mungu alipowaokoa Lutu na familia yake kutoka Sodoma, na matokeo yake hukumu ilimpitia ya kuwa nguzo ya chumvi, yeye alikamatwa na maisha ya zamani, badala ya kuyasahau yaliyipita alishikamana nayo na yakaharibu hatima yake, hatima yako inaweza kuathiriwa na mambo ya nyuma

Mwanzo 19:16-26 “Akakawia-kawia; nao wale watu wakamshika mkono, na mkono wa mkewe, na mkono wa binti zake wawili, kwa jinsi BWANA alivyomhurumia, wakamtoa wakamweka nje ya mji. Ikawa walipomtoa nje, mmoja alisema, Jiponye nafsi yako usitazame nyuma, wala usisimame katika hilo bonde po pote; ujiponye mlimani, usije ukapotea. Lutu akawaambia, Sivyo, bwana wangu! Tazama, mtumwa wako ameona kibali machoni pako, nawe umezidisha rehema zako ulizonifanyia kwa kuponya nafsi yangu, nami siwezi kukimbilia mlimani nisipatwe na yale mabaya, nikafa. Basi mji huu u karibu, niukimbilie, nao ni mdogo, nijiponye sasa huko, sio mdogo huu? Na nafsi yangu itaishi. Akamwambia, Tazama, nimekukubali hata kwa neno hili, kwamba sitauangamiza mji huo uliounena. Hima, ujiponye huko, maana siwezi kufanya neno lo lote, hata uingiapo humo. Kwa hiyo jina la mji ule likaitwa Soari. Jua lilikuwa limechomoza juu ya nchi Lutu alipoingia Soari. Ndipo BWANA akanyesha juu ya Sodoma na juu ya Gomora kiberiti na moto toka mbinguni kwa BWANA. Akaangusha miji hiyo na Bonde lote, na wote waliokaa katika miji hiyo, na yote yaliyomea katika nchi ile. Lakini mkewe Lutu akatazama nyuma yake, akawa nguzo ya chumvi.”

Luka 9:62 “Yesu akamwambia, Mtu aliyetia mkono wake kulima, kisha akaangalia nyuma, hafai kwa ufalme wa Mungu.”

Siri ya maisha ya ushindi iko katika kuyachuchumilia yaliyo mbele na kusahau yaliyo nyuma kama mtu anataka kusonaga mbele ni lazima asahau kushindwa kwake, asahau maumivu yote ya nyuma, asamehe endapo wako watu waliomuumiza, asahau majuto na aibu, asahau mafanikio yanayokufanya ujivune na kupata kiburi,  sahau hata watu ambao walikuwa karibu nawe na makusudi ya kuwa karibu nao yameisha, na umwangalie Yesu Kristo zaidi kwaajili ya mafanikio yako ya baadae , unapoyachuchumilia yaliyo mbele unafungua mlango mpya  na mlango huo unakufanya ukimbie mbio zako na kuufikia mwisho wenye ushindi na Mungu atakupa nguvu ya kukimbia hadi mwisho.

Athari za kutoyasahau yaliyo nyuma.

Wakati wowote watu wanapoangalia nyuma wanakuwa watumwa wa yaliyopita, Kristo alitukomboa ili tuishi maisha mapya yenye tumaini na uhuru yasiyo na hofu kwa hiyo kutokuyasahau yaliyo nyuma kunaathiri maisha yako

1.       Kunakufanya usiendelee kiroho, kimwili na kisaikolojia kwa sababu unaweza kukwama na hatia aibu au majuto,  na ukajiona hustahili Baraka mpya za Mungu, au ukabweteka na kile ulicho nacho!

2.       Kunakufanya uharibu furaha ya sasa – badala ya kumshukuru Mungu kwa yaliyopo na kukusaidia kusonga mbele unabaki unalilia yaliyopita  au unaridhika  na kile unachiokiona!

3.       Kutosahau yaliyo nyuma kunakufanya usiweze kuyafikia malengo mfano Paulo alikuwa analenga la kufika mbinguni na kupata thawabu na kukaa na bwana milele

4.       Kutokuyasahu yaliyo nyuma kunakufanya uwe mwoga wa hatua mpya – unashikwa na hofu ya kushindwa au unajutia mafanikio yaliyopita

5.       Kutoyasahau yaliyo nyuma kunakufanya uishi wakati uliopita badala ya wakati wa sasa wa kusudi la Mungu

Paulo alichagua neno moja tu kuyasahau yaliyopita na kuyachuchumilia yaliyo mbele hii ndio siri ya ushindi inayotoa ujasiri na kukufanya usiogope lolote, Neno la Mungu linatoa wito leo kuwa ni lazima usahahu kushindwa kwako, usahahu mafanikio yako ya nyuma, sahahu aibu, au kujilinganisha na wengine sahahu maumivu yako, usiishi katika majuto angalia mbele na Mungu atakutokea, kama unahitaji mafanikio makubwa zaidi chuchumilia yaliyo mbele!

Kumbukumbu 31:8 “Naye Bwana, yeye ndiye atakayekutangulia, atakuwa pamoja nawe, hatakupungukia wala kukuacha; usiogope wala usifadhaike.”     

Mithali 4:25-27 “Macho yako yatazame mbele, Na kope zako zitazame mbele yako sawasawa. Ulisawazishe pito la mguu wako, Na njia zako zote zithibitike; Usigeuke kwa kuume wala kwa kushoto; Ondoa mguu wako maovuni.

Rev. Innocent Samuel Kamote

Mkuu wa wajenzi mwenye hekima

Jumapili, 5 Aprili 2026

Kupandishwa toka shimo la uharibifu!


Zaburi 40:1-3 “Nalimngoja Bwana kwa saburi, Akaniinamia akakisikia kilio changu. Akanipandisha toka shimo la uharibifu, Toka udongo wa utelezi; Akaisimamisha miguu yangu mwambani, Akaziimarisha hatua zangu. Akatia wimbo mpya kinywani mwangu, Ndio sifa zake Mungu wetu. Wengi wataona na kuogopa, Nao watamtumaini Bwana




Utangulizi:

Ni muhimu kufahamu kwamba tuwapo duniani ziko nyakati ambazo tunaweza kupita katika mazingira ya hatari sana, mazingira ya kutisha ambayo kimsingi yanaweza kukuweka katika hali ya kukosa msaada wala hata kusikilizwa kwa sauti yako na ukakosa msaada ni nyakati ambazo unaweza kuchagua kifo kuliko uhai, wakati ambao unaweza kuchagua kukata tamaa kuliko kujipa moyo, nyakati ambazo umezama katika giza na huoni hata dalili ya nuru unachokiona mbele yako ni dalili za uharibifu yaani mauti, hali hiyo inaweza kuwa misiba, inaweza kuwa upotevu wa mali, inaweza kuwa kutapeliwa fedha nyingi, inaweza kuwa changamoto za kiafya inaweza kuwa mashambulizi kutoka kwa maadui, watu wanaokuchukia, inaweza kuwa magonjwa makubwa yasiyo na tiba na kadhalika hayo yanapokushambulia katika lugha ya kibiblia linaitwa shimo la uharibifu, katika nyakati hizo hata Mungu huonekana kuwa kimya unaweza ukamuita na ukasubiri na bado akakunyamazia, kipindi hicho huwa ni kipindi kigumu sana kwa mwanadamu na waandishi wa mashairi ya kibiblia wamekiita shimo la uharibifu! Je umewahi kupita au je unapita katika shimo la uharibifu? wako watu walipita

Zaburi 40:1-3 “Nalimngoja Bwana kwa saburi, Akaniinamia akakisikia kilio changu. Akanipandisha toka shimo la uharibifu, Toka udongo wa utelezi; Akaisimamisha miguu yangu mwambani, Akaziimarisha hatua zangu. Akatia wimbo mpya kinywani mwangu, Ndio sifa zake Mungu wetu. Wengi wataona na kuogopa, Nao watamtumaini Bwana

Katika maandiko yetu ya msingi, tunajifunza ushudua wa Daudi mwandishi wa zaburi hii akimshukuru Mungu baada ya kumuokoa na kumtoa katika shimo la uharibifu, lenye matope na uterezi, kuimarisha hatua zake na kutia wimbo mpya kinywani mwake, Pamoja na kuwa zaburi hii ilimuhusu Daudi, inamuhusu vile vile Yesu Kristo ambaye aliteswa akafa na kuzikwa na kufufuka siku ya tatu akitolewa katika shimo la uharibifu (kaburi), sio hivyo tu zaburi hii inamuhakikishia kila mmoja wetu kuwa Mungu atakutoa katika shimo la uharibifu unalolipitia, tutajifunza somo hili Akanipandisha toka shimo la uharibifu!  kwa kuzingatia vipengele vikuu muhimu vitatu vifuatavyo;-


·         Maana ya shimo la uharibifu

·         Kupandishwa toka shimo la uharibifu

·         Mamlaka ya kupandishwa toka shimoni  


Maana ya shimo la uharibifu.

Shimo la uharibifu katika lugha ya Kiebrania linaitwa “Shâ’ôn bôr” kwa kiingereza ni “Horrible pit” au  “Destruction bore”, au “tumult Pit” au “Sheol” kuzimu au kaburi au hatari ya kifo, ambalo maana yake ni shimo lenye kutisha, au shimo la uharibifu, au shimo la mateso, lenye kelele, lenye kuchanganya, Mwandishi anajaribu kusimulia hali ngumu ambayo Mungu anaweza kuiacha mtu wake akaipitia ambayo kimsingi, ni hali ya shinikizo kubwa sana la mateso ambayo kibinadamu ni vigumu kuyaepuka ni shimo ambalo unanasa na huwezi kujiokoa shimo la utelezi, shimo hili ni kama kuingizwa kaburini ukiwa umekufa ambako sio rahisi kutoka kwa nguvu zako na akili zako za kibinadamu mpaka kwa msaada wa Mungu, Ni Mungu peke yake ndiye anayeweza kukutoa huko!

Zaburi 28:1-2 “Ee Bwana, nitakuita Wewe, mwamba wangu, Usiwe kwangu kama kiziwi. Nisije nikafanana nao washukao SHIMONI, Ikiwa umeninyamalia. Uisikie sauti ya dua yangu nikuombapo, Nikipainulia patakatifu pako mikono yangu.”

Zaburi 88:3-6 “Maana nafsi yangu imeshiba taabu, Na uhai wangu umekaribia kuzimu. Nimehesabiwa pamoja nao washukao SHIMONI; Nimekuwa kama mtu asiye na msaada. Miongoni mwao waliokufa nimetupwa, Kama waliouawa walalao makaburini. Hao ambao Wewe huwakumbuki tena, Wametengwa mbali na mkono wako. Mimi umenilaza katika shimo la chini, Katika mahali penye giza vilindini.”

Zaburi 30:1-3 “Ee Bwana, nitakutukuza kwa maana umeniinua, Wala hukuwafurahisha adui zangu juu yangu. Ee Bwana, Mungu wangu, Nalikulilia ukaniponya. Umeniinua nafsi yangu, Ee Bwana, kutoka KUZIMU. Umenihuisha na kunitoa Miongoni mwao washukao SHIMONI.”

Isaya 38:17-18 “Tazama; nalikuwa na uchungu mwingi kwa ajili ya amani yangu; Lakini kwa kunipenda umeniokoa na SHIMO LA UHARIBIFU; Kwa maana umezitupa dhambi zangu zote nyuma yako. Kwa kuwa KUZIMU hakuwezi kukusifu; mauti haiwezi kukuadhimisha; Wale washukao SHIMONI hawawezi kuitarajia kweli yako.”

Unaona neno shimo katika maandiko au shimo la uharibifu linazungumzia hali ya hatari, hali ya mateso makali, kukata tamaa, hali ya kushindwa na kukandamizwa ni shida na taabu ambazo zinaelekea kelele za mauti na wakati huohuo huwezi kujiokoa au kujitoa katika shimo hilo kwa kuwa ni shimo la matope, hali hii inaweza kufanana kabisa na hali ya mateso aliyoyapitia Bwana wetu Yesu Kristo na kufa kwake msalabani ambapo hakupata msaada wowote wakati wa mateso, kwa hiyo wakati mwingine tunapitia hali kama hiyo ambayo kimsingi tunaweza kufikia kukata tamaa, shimo hili linaweza kuwa shimo la madeni, linaweza kuwa shimo la umasikini, linaweza kuwa shimo la magonjwa, linaweza kuwa shimo la msongo wa mawazo, linaweza kuwa shimo la dhambi, linaweza kuwa shimo la mauti, linaweza kuwa shimo la kushindwa kiroho, linaweza kuwa la matatizo

Kupandishwa toka shimo la uharibifu.

Tunapoadhimisha msimu huu wa pasaka na kufufuka kwa Bwana wetu Yesu Kristo kutoka kwa wafu, tunajikumbusha vile vile kazi ya Mungu ya kuwatoa wanadamu kutoka katika mashimo ya uharibifu mashimo ambayo huwezi kujitoa bila nguvu ya ufufuo, kukutoa katika shimo lako, Yesu alipokufa aliwekwa shimoni na adui zake walililinda na kaburi ili kuhakikisha ya kuwa hatoki humo, Yesu aliingia katika shimo la mateso, alikataliwa na watu jamii nzima ilizomewa jamii ikisema asulubiwe asulubiwe, alipigwa mijeledi, na kuwambwa msalabani akiwa uchi na kufa msalabani na kuzikwa mahali pa giza nene, kaburi lake na mateso yake yalikuwa ni alama ya aibu, kifo, na kushindwa katika macho ya wanadamu, wanadamu wakikuchukia ni kawaida yao kukuweka shimoni

-          Walimuweka Yusufu katika shimo la matope Mwanzo 37:18-24 “Wakamwona toka mbali, na kabla hajawakaribia, wakafanya shauri juu yake ili wamwue. Wakasemezana wao kwa wao, Tazama, yule bwana wa ndoto anakuja. Haya, twende, tukamwue na kumtupa katika birika mojawapo, nasi tutasema, Mnyama mkali amemla; kisha tutaona zitakuwaje ndoto zake. Reubeni akasikia akamwokoa katika mikono yao, akasema, Tusimwue. Reubeni akawaambia, Msimwage damu; mtupeni katika birika hii iliyopo nyikani, wala msimguse; ili apate kumwokoa katika mikono yao, akamrudishe kwa baba yake. Ikawa Yusufu alipofika kwa ndugu zake, wakamvua Yusufu kanzu yake, kanzu ile ndefu aliyoivaa, wakamtwaa wakamtupa katika birika; na hiyo birika ilikuwa tupu, hamna maji.”

 

-          Walimuweka Yeremia katika shimo la matope Yeremia 38:6-9 “Basi wakamtwaa Yeremia, wakamtupa katika shimo la Malkiya, mwana wa mfalme, lililo katika uwanda wa walinzi; wakamshusha kwa kamba. Na mle shimoni hamkuwa na maji, ila matope tu; naye Yeremia akazama katika matope hayo. Basi, Ebedmeleki, Mkushi, towashi, aliyekuwa katika nyumba ya mfalme, aliposikia kama wamemtia Yeremia shimoni; na wakati huo mfalme alikuwa amekaa katika lango la Benyamini; Ebedmeleki akatoka nyumbani mwa mfalme, akamwambia mfalme, akisema,Ee bwana wangu, mfalme, watu hawa wametenda mabaya katika mambo yote waliyomtenda Yeremia, nabii, ambaye wamemtupa shimoni; naye hakosi atakufa pale alipo, kwa sababu ya njaa; kwa kuwa hapana mkate kabisa katika mji.”         

 

-          Walimtupa Daniel katika shimo lenye simba wakali Daniel 6:16-17 “Basi mfalme akatoa amri, nao wakamleta Danieli, wakamtupa katika tundu la simba. Mfalme akanena, akamwambia Danieli, Mungu wako unayemtumikia daima, yeye atakuponya. Likaletwa jiwe, likawekwa mdomoni mwa lile tundu; naye mfalme akalitia muhuri kwa muhuri yake mwenyewe, na kwa muhuri ya wakuu wake, lisibadilike neno lo lote katika habari za Danieli.”

 

Wote waliowekwa shimoni hapo juu walichukiwa, walikataliwa walifanyiwa hila na njama ili ikiwezekana waweze kumalizwa na wasitoke lakini Mungu alikuwa pamoja nao, Daudi pia aliishi mashimoni yaani katika mapango  akitafutwa kuuawa, Yesu Kristo aliwekwa kwenye shimo yaani kaburi, na liliwekwa Muhuri kama la Daniel wote walikuwa wanakabiliwa na mauti, walikandamizwa, walionewa, waliteswa Neno la Mungu linaonyesha ya kuwa ni Mungu mwenyewe ndiye aliyewatoa kutoka katika shimo la uharibifu kama mwandishi wa Zaburi anavyosema

Zaburi 40:1-3 “Nalimngoja Bwana kwa saburi, Akaniinamia akakisikia kilio changu. Akanipandisha toka shimo la uharibifu, Toka udongo wa utelezi; Akaisimamisha miguu yangu mwambani, Akaziimarisha hatua zangu. Akatia wimbo mpya kinywani mwangu, Ndio sifa zake Mungu wetu. Wengi wataona na kuogopa, Nao watamtumaini Bwana

Wakati wa shida yako unapopita katika shimo la uharibifu unaweza kuliitia jina la Bwana naye atakuokoa kutoka shimoni uwezo huo na mamlaka hiyo ya kumtoa mtu kutoka shimoni iko mikononi mwa Mungu, Mwandishi wa zaburi alikuwa katika wakati mgumu aliliitia jina la Bwana na Mungu akikuwa kimya kwa Muda lakini baadae alimchungulia na kisha akamtoa akaimarisha hatua zake, akamuweka juu ya mwamba na kisha akatia wimbo mpya, ni maombi yangu pasaka hii iwe ushuhuda  

Ayubu 33:23-24 “Kwamba akiwapo malaika pamoja naye, Mkalimani, mmoja katika elfu, Ili kumwonyesha binadamu hayo yampasayo; Ndipo amwoneapo rehema, na kusema, Mwokoe asishuke SHIMONI; Mimi nimeuona ukombozi.”

Ayubu 33:28-30 “Yeye ameikomboa nafsi yangu isiende SHIMONI, Na uhai wangu utautazama mwanga. Tazama, hayo yote ni Mungu anayeyafanya, Mara mbili, naam, hata mara tatu, kwa mtu, Ili kurudisha roho yake itoke SHIMONI, Ili atiwe mwanga kwa mwanga wa walio hai.

Yona 2:5-6 “Maji yalinizunguka, hata nafsini mwangu; Vilindi vilinizunguka; Mwani ulikizinga kichwa changu; Nalishuka hata pande za chini za milima; Hiyo nchi na mapingo yake yalinifunga hata milele; Lakini umeipandisha nafsi yangu kutoka SHIMONI, Ee Bwana, Mungu wangu,”

Zaburi 103:3-4 “Akusamehe maovu yako yote, Akuponya magonjwa yako yote, Aukomboa uhai wako na KABURI, Akutia taji ya fadhili na rehema,”          

Mamlaka ya kupandishwa toka shimoni 

Zaburi 40:1-3 “Nalimngoja Bwana kwa saburi, Akaniinamia akakisikia kilio changu. Akanipandisha toka shimo la uharibifu, Toka udongo wa utelezi; Akaisimamisha miguu yangu mwambani, Akaziimarisha hatua zangu. Akatia wimbo mpya kinywani mwangu, Ndio sifa zake Mungu wetu. Wengi wataona na kuogopa, Nao watamtumaini Bwana

Mwandishi wa Zaburi hii yaani Daudi anaonyesha ya kuwa hakuna mwingine anayeweza kumtoa mtu katika shimo la uharibifu isipokuwa Bwana mwenyewe kwa hiyo anasema alimgoja Bwana kwa uvumilivu yaani kwa Saburi, ukombozi wetu unaanza pale tunapoliitia jina la Bwana na kuvumilia yeye ndiye mwenye mamlaka ya kukuchomoa kutoka katika shimo lenye matope, lenye utelezi, yeye anayo mamlaka ya kukutoa katika minyororo, na mazingira yoyote magumu na kubadilisha yale yasiyowezekana na yakawezekana, Hakuna shimo lolote ambalo linaweza kuwa refu kuliko mkono wa Mungu, Mungu anapokutoa hukuweka juu ya mwamba na kuimarisha hatua zako na kukupa ushuhuda mpya wimbo mpya na kila mtu atajifunza kutoka kwako na watu watamtumaini na kumtegemea Mungu, shimo lolote la kushindwa, shimo la dhambi, shimo la mauti, shimo la kukata tamaa, shimo mateso, shimo la madeni, shimo la uharibifu, shimo la aibu, na changamoto.

Katika jina la Yesu Kristo, mwenye mamlaka ya mauti na uzima, mwenye ufunguo wa Daudi naamuru kila mmoja aliyewekwa katika shimo la uharibifu shimo hilo likuachie haraka, shimo la mapepo, shimo la uchawi, shimo la madeni, shimo la kukataliwa, shimo la kusalitiwa, shimo la kuonewa, shimo  la mafarakano, shimo la talaka, shimo na uharibifu katika ndoa, shimo la uharibifu katika familia,  shimo la utumwa wadhambi, shimo la magonjwa sugu, shimo la uonevu naamuru katika jina la Yesu Kristo aliyefufuka kutoka kwa wafu, kila shimo lililokumeza likutapike likuachie katika jina la Yesu Kristo wa Nazareth aliye hai, Bwana akuchomoe katika shimo la matope kama Mchungaji anavyomchomoa Kondoo wake katika jina la Yesu Kristo mwana wa Mungu aliye hai Amen!

Na. Rev. Innocent Samuel Kamote

Mkuu wa wajenzi mwenye Hekima 

Ijumaa, 3 Aprili 2026

Hana umbo wala uzuri hata tumtamani!

 


Isaya 53:2-5 “Maana alikua mbele zake kama mche mwororo, Na kama mzizi katika nchi kavu; Yeye hana umbo wala uzuri; Na tumwonapo hana uzuri hata tumtamani. Alidharauliwa na kukataliwa na watu; Mtu wa huzuni nyingi, ajuaye sikitiko; Na kama mtu ambaye watu humficha nyuso zao, Alidharauliwa wala hatukumhesabu kuwa kitu. Hakika ameyachukua masikitiko yetu, Amejitwika huzuni zetu; Lakini tulimdhania ya kuwa amepigwa, Amepigwa na Mungu, na kuteswa. Bali alijeruhiwa kwa makosa yetu, Alichubuliwa kwa maovu yetu; Adhabu ya amani yetu ilikuwa juu yake, Na kwa kupigwa kwake sisi tumepona.”




Utangulizi:

Leo ni siku ya Ijumaa kuu! Wakristo wote Nchini wanaungana na wakristo wote duniani kukumbuka na kuadhimisha kuteswa, kusulubiwa na kufa msalabani kwa Yesu Kristo wa Nazareth kulikotokea huko nje ya Yerusalem Israel miaka zaidi ya 2000 iliyopita, Katika kujikumbusha tukio hilo kama lilivyotabiriwa na Nabii Isaya zaidi ya miaka 700 kabla ya kuzaliwa kwake, Mateso yake haya yalifanyika dhidi yake huku akiwa hakufanya kosa lolote, lakini maandiko yanaeleza kuwa yalimkuta hayo kwaajili ya uponyaji wa wanadamu kwa sababu imeandika kwa kupigwa kwake sisi tumepona

1Petro 2:22-24 “Yeye hakutenda dhambi, wala hila haikuonekana kinywani mwake. Yeye alipotukanwa, hakurudisha matukano; alipoteswa, hakuogofya; bali alijikabidhi kwake yeye ahukumuye kwa haki. Yeye mwenyewe alizichukua dhambi zetu katika mwili wake juu ya mti, tukiwa wafu kwa mambo ya dhambi, tuwe hai kwa mambo ya haki; na kwa kupigwa kwake mliponywa.”

Kwa msingi huo basi leo tutachukua muda kutafakari na kujifunza kwa kina somo hili “HANA UMBO WALA UZURI HATA TUMTAMANI” kwa kuzingatia vipengele vikuu vitatu muhimu vifuatavyo:-


·         Maana ya neno hana umbo wala uzuri hata tumtamani

·         Yeye hana umbo wala uzuri hata tumtamani

·         Faida ya Mateso ya Bwana wetu Yesu Kristo 


Maana ya neno hana umbo wala uzuri hata tumtamani.

Ni muhimu kufahamu kuwa nabii Isaya alitabiri kuhusu mateso ya Yesu Kristo miaka 700 kabla ya Kristo kuzaliwa na hatimaye unabii wake ulikuja kutimizwa, akimuona katika kioo cha kinabii Isaya anasema kuhusu Masihi katika mateso yake “Yeye hana umbo wala uzuri; Na tumwonapo hana uzuri hata tumtamani.” Maneno haya yana maana gani sasa hebu tuyarejee tena.

Isaya 53:2 “Maana alikua mbele zake kama mche mwororo, Na kama mzizi katika nchi kavu; Yeye hana umbo wala uzuri; Na tumwonapo hana uzuri hata tumtamani.”  

Maneno haya hayamaanishi kamwe kuwa Yesu hakuwa mzuri au hakuwa na mvuto wa kimwili hapana Yesu alikuwa mzuri sana na kijana mwenye mvuto wa kupita kawaida, lakini Isaya anamuona katika kipindi cha mateso yake Yesu akiwa ameharibiwa vibaya na kuchakazwa katika sehemu zote muhimu za mwili wa kibinanadamu, Neno la Kiebrania linalotumika kuelezea umbo ni “tô’ar” na uzuri ni “Hâdâr” ambayo kwa kiingereza ni “appearance” na “majesty” maana yake ni kuwa mwili wake uliharibiwa vibaya sana “disfigured” na heshima yake au utukufu wake ulidhalilishwa na kushushwa kupita maelezo “dishonoured”  kwa hiyo Isaya ni kama anaelezea kuwa wakati wa mateso yake Yesu Kristo hakuna mtu angeweza kutamani kumuona, mateso yale yaliharibu kabisa muonekano wake  na yalidhalilisha kabisa utu wake, hakuwa na utukufu wa kifalme, wala huwezi kutamani kumuona  na kwa sababu hiyo alidharauliwa sana, Mateso yake yalikuwa kama njia ya kumvunjia heshima na kumdhalilisha kabisa na kuharibu heshima yake waliomsulubisha sio tu walikuwa na uwepo wa kishetani lakini pia walimuonea wivu kutokana na uzuri aliokuwa nao na wakakusudia kuuharibu kwa hiyo chuki za waliomsulubisha pia na wivu ulihusika katika kuhakikisha kuwa wanamuharibu kabisa sura yake na kumvunjia kabisa Heshima yake anaelezea mwandishi wa historia wa kiyahudi wa Karne ya kwanza Flavours Josephus walitaka kuhakikisha kuwa anakuwa na huzuni na nafasi ya kujisikitikia

Isaya 53:3-4 “Alidharauliwa na kukataliwa na watu; Mtu wa huzuni nyingi, ajuaye sikitiko; Na kama mtu ambaye watu humficha nyuso zao, Alidharauliwa wala hatukumhesabu kuwa kitu. Hakika ameyachukua masikitiko yetu, Amejitwika huzuni zetu; Lakini tulimdhania ya kuwa amepigwa, Amepigwa na Mungu, na kuteswa.”

Yeye hana umbo wala uzuri hata tumtamani!

Kama tulivyoona maana ya kauli ya hana umbo wala uzuri hata tumtamani ambayo ina maanisha ule uzuri aliokuwa nao Yesu Kristo na utukufu wake uliweza kuharibiwa vibaya kiasi ambacho mtu hangeweza kufikiri kuwa huyu ni mtu au ni mwanadamu yaani aliharibiwa katika namna ambayo ni ngumu kujua kuwa huyu ni mtu yaani watesi walihakikisha wanambomoa uso wake na mwili wake na nafsi yake na roho yake maandiko yanaeleza kuwa aliharibiwa katika kiwango ambacho hakuna mwanadamu aliwahi kuharibiwa hivyo

Isaya 52:14 “Kama vile wengi walivyokustaajabia, (uso wake ulikuwa umeharibiwa sana zaidi ya mtu ye yote, na umbo lake zaidi ya wanadamu),

Isaya 53:5 “Bali alijeruhiwa kwa makosa yetu, Alichubuliwa kwa maovu yetu; Adhabu ya amani yetu ilikuwa juu yake, Na kwa kupigwa kwake sisi tumepona.”    

Watesi wa Yesu Kristo walihakikisha kuwa Yesu anateseka kwa namna zote, anateseka kihisia, kimwili, kijamii, kiroho na kisaikolojia, walimuharibu na kuuchakaza mwili wake kwa mateso ambayo Biblia inaeleza hakuna mtu alichakazwa kwa mtindo na mfumo kama aliofanyiwa Yesu, inawezekana filamu ya “Passion of Christ” ikawa imeonyesha kwa kiwango Fulani uhalisia wa mateso yake, maandiko yakisema aliharibiwa ujue aliharibiwa kweli!  

Kihisia – Yesu alikataliwa na watu wake, alisalitiwa na Yuda Iskariote, kisha wanafunzi wake walimkimbia na wakati wa mateso alibaki peke yake, Petro alimkana mara tatu, mateso haya yakiongozwa na uwepo wa kishetani yalikuwa ni kwaajili ya kusababisha manung’uniko katika moyo wa Yesu apate maumivu ya kihisia na kudhalilika

Yohana 1:10-11 “Alikuwako ulimwenguni, hata kwa yeye ulimwengu ulipata kuwako, wala ulimwengu haukumtambua. Alikuja kwake, wala walio wake hawakumpokea

Mathayo 26:14-16 “Wakati huo mmoja wa wale Thenashara, jina lake Yuda Iskariote, aliwaendea wakuu wa makuhani, akasema, Ni nini mtakachonipa, nami nitamsaliti kwenu? Wakampimia vipande thelathini vya fedha. Tokea wakati huo akawa akitafuta nafasi apate kumsaliti.            

Mathayo 26:56 “Lakini haya yote yamekuwa, ili maandiko ya manabii yatimizwe. Ndipo wanafunzi wote wakamwacha, wakakimbia.”

Luka 22:59-61 “Halafu, yapata saa moja, mtu mwingine alikaza kusema, Hakika na huyu alikuwa pamoja naye, kwa kuwa yeye pia ni Mgalilaya. Petro akasema, Ee mtu, sijui usemalo. Na papo hapo alipokuwa katika kusema, jogoo aliwika. Bwana akageuka akamtazama Petro. Petro akalikumbuka lile neno la Bwana jinsi alivyomwambia, Leo kabla hajawika jogoo utanikana mara tatu.”

Kimwili – Maandiko yanaonyesha kuwa mtumishi wa Mungu (Yesu Kristo) angeteswa katika kiwango ambacho asingeliweza kutambulika, askari wa kirumi walikuwa kama wenye mzuka au walipagawa lilipokuja swala la mateso ya Kristo, walimpiga mijeledi mingi katika namna isiyoweza kuhesabika, walimvika taji ya miiba, huku wakimpiga makofi na kumtemea mate, aliwambwa msalabani akisulubiwa mikono na miguu, kimsingi hakuna mateso makali kama kusulubiwa msalabani, lakini kabla ya hilo wanajeshi wa kirumi walishika mijeledi na kumfunga Yesu kwenye kizimba ambapo unavuliwa nguo na kutandikwa mijeledi, Mijeledi ilikuwa ni fimbo yenye nyuzi kumi na mbili na zile nyuzi zilikuwa na vipande vya vyuma na mifupa ya wanyama wagumu, askari wawili wanaume wenye nguvu walitandika kwa kushindana na wengi waliopitia adhabu hii walichanika tumbo na utumbo ulimwagika nje, unabii wa Isaya na ule wa Daudi katika Zaburi unathibitisha hali mbaya ya mateso ya Kristo namna alivyokuwa

Zaburi 22:14-18 “Nimemwagika kama maji, Mifupa yangu yote imeteguka, Moyo wangu umekuwa kama nta, Na kuyeyuka ndani ya mtima wangu. Nguvu zangu zimekauka kama gae, Ulimi wangu waambatana na taya zangu; Unaniweka katika mavumbi ya mauti, Kwa maana mbwa wamenizunguka; Kusanyiko la waovu wamenisonga; Wamenizua mikono na miguu. Naweza kuihesabu mifupa yangu yote; Wao wananitazama na kunikodolea macho. Wanagawanya nguo zangu, Na vazi langu wanalipigia kura.”             

Yohana 19:1-3 “Basi ndipo Pilato alipomtwaa Yesu, akampiga mijeledi. Nao askari wakasokota taji ya miiba, wakamtia kichwani, wakamvika vazi la zambarau. Wakawa wakimwendea, wakisema, Salamu! Mfalme wa Wayahudi! Wakampiga makofi.”

Mathayo 26:67-68 “Ndipo wakamtemea mate ya uso, wakampiga makonde; wengine wakampiga makofi, wakisema, Ewe Kristo, tufumbulie; ni nani aliyekupiga?

Mathayo 27:29-31 “Wakasokota taji ya miiba, wakaiweka juu ya kichwa chake, na mwanzi katika mkono wake wa kuume; wakapiga magoti mbele yake, wakamdhihaki, wakisema, Salamu, Mfalme wa Wayahudi! Kisha wakamtemea mate, wakautwaa ule mwanzi, wakampiga-piga kichwani. Walipokwisha kumdhihaki, wakalivua lile vazi, wakamvika mavazi yake, wakamchukua kumsulibisha.”

Kijamii - Yesu aliteswa kijamii. Alidhihakiwa hadharani dhidi ya watu wale waliokuwa wakimuheshimu, alihesabiwa pamoja na wahalifu yeye akiwekwa kati kati yao, lakini alivuliwa nguo hadharani tukio hili lilikuwa la udhalilishaji na uaibishaji , jamii hiyo hiyo wakati wa hukumu yake walipiga kelele wakisema asulubiwe asulubiwe!

Isaya 53:12 “Kwa hiyo nitamgawia sehemu pamoja na wakuu, Naye atagawanya nyara pamoja nao walio hodari; Kwa sababu alimwaga nafsi yake hata kufa, Akahesabiwa pamoja na hao wakosao. Walakini alichukua dhambi za watu wengi, Na kuwaombea wakosaji.”        

Yohana 19:23 “Nao askari walipomsulibisha Yesu, waliyatwaa mavazi yake, wakafanya mafungu manne, kwa kila askari fungu lake; na kanzu nayo. Basi kanzu ile haikushonwa, ilikuwa imefumwa yote pia tangu juu.”

Kiroho – kwa kuwa alikuwa amezibeba dhambi za ulimwengu mzima, kwa wakati ule Mungu alikuwa amemuacha, kwa hiyo kwa wakati ule ilikuwa ni kama Mungu amemuacha na kumtenga, Mungu hakumwangalia kama mwanae!

Isaya 59:1-2 “Tazama, mkono wa Bwana haukupunguka, hata usiweze kuokoa wala sikio lake si zito, hata lisiweze kusikia; lakini maovu yenu yamewafarikisha ninyi na Mungu wenu, na dhambi zenu zimeuficha uso wake msiuone, hata hataki kusikia.            

Mathayo 27:45-46 “Basi tangu saa sita palikuwa na giza juu ya nchi yote hata saa tisa. Na kama saa tisa, Yesu akapaza sauti yake kwa nguvu akisema, Eloi, Eloi, lama sabakthani? Yaani, Mungu wangu, Mungu wangu, mbona umeniacha?                         

Faida ya Mateso ya Bwana wetu Yesu Kristo.

Tunapoadhimisha mateso ya Bwana wetu Yesu Kristo aliyeyatoa maisha yake kufa msalabani ni muhimu kwetu kufahamu kuwa Yesu alikubali kufa Msalabani na kuharibiwa vibaya katika namna tuliyojifunza kwa sababu ya makosa yetu na maovu yetu na kwaajili ya tukio hili ziko faida nyingi zinazopatikana kwa kufa kwake Msalabani.

Isaya 53:4-5 “Hakika ameyachukua masikitiko yetu, Amejitwika huzuni zetu; Lakini tulimdhania ya kuwa amepigwa, Amepigwa na Mungu, na kuteswa. Bali alijeruhiwa kwa makosa yetu, Alichubuliwa kwa maovu yetu; Adhabu ya amani yetu ilikuwa juu yake, Na kwa kupigwa kwake sisi tumepona.”

Kwa tendo la Yesu Kristo kufa Msalabani, alizibeba dhambi zetu, na kuwapatanisha wanadamu kwa Mungu kwa kuondoa kiambaza kilichokuwepo kati yetu na Mungu na sio hivyo tu bali aliziharibu nguvu za shetani za kupata mashiko ya kutushitaki akituletea uponyaji wa mwili nafsi na roho lakini kuu kuliko yote ni uzima wa milele

-          Tunapata msamaha wa dhambi kwa sababu aliimwaga damu yake pale msalabani na pasipo kumwagika damu hakuna ondoleo la dhambi

 

Waebrania 9:22 “Na katika Torati karibu vitu vyote husafishwa kwa damu, na pasipo kumwaga damu hakuna ondoleo.”

 

-          Tunapata uponyaji wa mwili nasfi na roho kwa sababu mateso yake yalibeba na kusulubisha magonjwa yetu, maumivu yetu na udhaifu wetu

 

1Petro 2:24 “Yeye mwenyewe alizichukua dhambi zetu katika mwili wake juu ya mti, tukiwa wafu kwa mambo ya dhambi, tuwe hai kwa mambo ya haki; na kwa kupigwa kwake mliponywa.”

 

-          Tunapata Amani ya ndani kabisa iliyopotea, Kila mtu aliyempokea Yesu hata pamoja na kupitia changamoto za aina mbalimbali duniani utaweza kugundua kuwa anapewa Amani ya ndani sana ambayo kimsingi gharama zake zililipwa pale msalabani adhabu aliyopewa ilituletea sisi Amani ya kweli ya maisha ya ndani sana na mwanadamu

 

Amani Isaya 53:4-5 “Hakika ameyachukua masikitiko yetu, Amejitwika huzuni zetu; Lakini tulimdhania ya kuwa amepigwa, Amepigwa na Mungu, na kuteswa. Bali alijeruhiwa kwa makosa yetu, Alichubuliwa kwa maovu yetu; Adhabu ya amani yetu ilikuwa juu yake, Na kwa kupigwa kwake sisi tumepona.”

 

-          Tunaupata ushindi dhidi ya shetani na nguvu zake zote za giza, tendo la kufa kwa Yesu Kristio msalabani baada ya kusulubiwa kwake maaana yake alizivua  enzi  na mamlaka yaani nguvu zake na utendaji wake shetani

 

Wakolosai 2:14-15 “akiisha kuifuta ile hati iliyoandikwa ya kutushitaki kwa hukumu zake, iliyokuwa na uadui kwetu; akaiondoa isiwepo tena, akaigongomea msalabani; akiisha kuzivua enzi na mamlaka, na kuzifanya kuwa mkogo kwa ujasiri, akizishangilia katika msalaba huo.”

 

-          Msalaba ni njia ya uzima huu na uzima wa milele, Kifo cha Yesu kimetuletea uzima wa mwili na uzima wa kiroho  kwa hiyo katika yeye tunao uzima wa milele

 

Yohana 10:10-11 “Mwivi haji ila aibe na kuchinja na kuharibu; mimi nalikuja ili wawe na uzima, kisha wawe nao tele. Mimi ndimi mchungaji mwema. Mchungaji mwema huutoa uhai wake kwa ajili ya kondoo.“

 

1Yohana 5:12-13 “Yeye aliye naye Mwana, anao huo uzima; asiye naye Mwana wa Mungu hana huo uzima. Nimewaandikia ninyi mambo hayo, ili mjue ya kuwa mna uzima wa milele, ninyi mnaoliamini Jina la Mwana wa Mungu.

Hitimisho

Wokovu una gharama kubwa sana umegharimu maisha ya mwana wa Mungu, hatuna budi kuujali na kutokuupuuzia ili tuweze kupona, aliharibiwa namna ile ili sisi tutengenezwe na kufaa mbele za Mungu, basi tuukubali wokovu.

Waebrania 2:2-4 “Kwa maana, ikiwa lile neno lililonenwa na malaika lilikuwa imara, na kila kosa na uasi ulipata ujira wa haki, sisi je! Tutapataje kupona, tusipojali wokovu mkuu namna hii? Ambao kwanza ulinenwa na Bwana, kisha ukathibitika kwetu na wale waliosikia; Mungu naye akishuhudu pamoja nao kwa ishara na ajabu na nguvu za namna nyingi, na kwa magawanyo ya Roho Mtakatifu, kama alivyopenda mwenyewe.”

Na. Rev. Innocent Samuel Kamote

Mkuu wa wajenzi mwenye Hekima       

Jumapili, 29 Machi 2026

Mtoto hajafa Amelala tu !


Marko 5:35-40 “Hata alipokuwa katika kunena, wakaja watu kutoka kwa yule mkuu wa sinagogi, wakisema, Binti yako amekwisha kufa; kwani kuzidi kumsumbua mwalimu? Lakini Yesu, alipolisikia lile neno likinenwa, akamwambia mkuu wa sinagogi, Usiogope, amini tu. Wala hakumruhusu mtu afuatane naye, ila Petro, na Yakobo, na Yohana nduguye Yakobo. Wakafika nyumbani kwa yule mkuu wa sinagogi, akaona ghasia, na watu wakilia, wakifanya maombolezo makuu. Alipokwisha kuingia, akawaambia, Mbona mnafanya ghasia na kulia? Kijana hakufa, bali amelala tu. Wakamcheka sana. Naye alipokwisha kuwatoa nje wote, akamtwaa babaye yule kijana na mamaye, na wale walio pamoja naye, akaingia ndani alimokuwamo yule kijana.



Utangulizi:

Kila mwanadamu mwenye akili timamu huwa anakuwa na ndoto na matarajio kadhaa wa kadha katika maisha, wengine huwa na matarajio makubwa wengine ya wastani na wengine ya kawaida tu katika maisha, kwa kawaida matarajio fulani yasipofikiwa au kutimia katika maisha husababisha msongo mkubwa wa mawazo na wakati mwingine kupoteza kabisa matumaini, matarajio hayo wakati mwingine yanaweza kuwa ya wazi na wakati mwingine yanaweza kuwa ya siri lakini kwa vyo vyote vile yasipofikiwa anayeumia zaidi ni yule aliyekuwa na matumaini hayo. Neno la Mungu lasema

Mithali 13:12 “Kilichotarajiwa kikikawia kuja, moyo huugua. Bali haja ya mtu ikipatikana, ni mti wa uzima.”

Hali hii ilimkuta mtu mmoja muhimu sana katika maandiko, huyu anatajwa kama mojawapo ya wakuu wa sinagogi ambaye alimwendea Yesu wakati binti yake mdogo akiwa katika hali ya kufa, ili yamkini ikiwezekana Yesu aweze kumuhudumia na kuokoa uhai wake aendelee na maisha naye

Marko 5:22-24 “Akaja mtu mmoja katika wakuu wa sinagogi, jina lake Yairo; hata alipomwona, akaanguka miguuni pake, akimsihi sana, akisema, Binti yangu mdogo yu katika kufa; nakuomba uje, uweke mkono wako juu yake, apate kupona, na kuishi. Akaenda pamoja naye; mkutano mkuu wakamfuata, wakimsonga-songa.”

Akiwa katika safari ya kuelekea kumhudumia Yesu alisongwa songwa na watu wengi waliokuwa wakihitaji huduma na zaidi sana tukio la mwanamke mmoja aliyekuwa anatokwa na damu kwa muda wa miaka 13 liliingilia kati na kwa sababu hiyo kuchelewesha safari ya Yesu kufika kwa Yairo, Akiwa katika huduma za dharula zilizokuwa zinaingilia kati, katika huduma za Yesu hapa linakuja kundi la watu na kumpasha habari Yairo kwamba asiendelee kumsumbua Mwalimu kwani binti yake amekwisha kufa!  

Marko 5:35 “Hata alipokuwa katika kunena, wakaja watu kutoka kwa yule mkuu wa sinagogi, wakisema, Binti yako amekwisha kufa; kwani kuzidi kumsumbua mwalimu?

Unapopiga picha ya kile kilichokuwa kinaendelea katika moyo wa Yairo utaweza kugundua kuwa kwa vyovyote vile moyo wake uliugua zaidi na nguvu zake zilimuishia na huenda alikata tamaa, hali kama hii huwapata  baadhi yetu pale yale tunayoyatarajia yanapoonekana kutokuwa na uwezo wa kutimia tena, hali ya kupoteza matumaini inatokea, ndoto zinapokufa, mambo yanapoonekana kutokwenda kama vile tulivyotarajia, afya inapokuwa hatarini, kazi inapoonekana kufika mwisho, mkataba unapoonekana kusimama, kazi uliyoitarajia inapoonekana kufikia mwisho, mchongo unaousikilizia unapoota mbawa, uchumba unapovunjika, mtaji unaposambaratika, mkopo unaposhindwa kulipwa, hasara katika biashara, mavuno usiyoyatarajia na kadhalika wakati huu matumaini huonekana kutoweka  na hiyo iko hivyo katika mtazamo wa Binadamu  Yesu anakuambia usilie kuna matumaini


·         Mungu huona tofauti na wanadamu.

·         Kelele za watu hazibadilishi mpango wa Mungu

·         Mtoto hajafa amelala tu    

          

Mungu huona tofauti na wanadamu

Matarajio ya kila mwanadamu anapopitia changamoto mbalimbali ni pamoja na suluhu ya haraka, kukosa faraja kukumbana na mipaka na kutamani kuondoka katika maumivu yanayotusibu, wakati Mungu mtazamo wake ni wa muda mrefu, wa kutukuza kiroho kutukomaza na kutaka tuuone utukufu wake lakini zaidi sana kuimarisha uhusiano wetu na yeye milele, wanadamu tunaona changamoto kama vikwazo njiani  wakati Mungu anaona vikwazo kama njia ya kuonyesha nguvu na utukufu wake, upendo wake na namna anavyotujali  lakini pia kunyamazisha kelele za kipinzani, wakati watu wanaona mauti kama jambo gumu sana na mwisho wa kila kitu, Yesu anaona mauti ni kama usingizi tu

Isaya 55:8-9 “Maana mawazo yangu si mawazo yenu, wala njia zenu si njia zangu; asema Bwana. Kwa maana kama vile mbingu zilivyo juu sana kuliko nchi, kadhalika njia zangu zi juu sana kuliko njia zenu, na mawazo yangu kuliko mawazo yenu.”

Wakati mwanadamu anawaza kuwa amefika mwisho, Mungu ndio kwanza anaanza jambo, wakati wanadamu wanafikiri kuwa haiwezekani, Mungu anaona kivingine wakati mwanadamu anaona mauti na ukavu, Mungu anaona uhai na upako, Mungu hatendi kazi kwa hisia bali kwa imani!

Ezekiel 37:1-3 “Mkono wa Bwana ulikuwa juu yangu, naye akanichukua nje katika roho ya Bwana, akaniweka chini, katikati ya bonde; nalo limejaa mifupa; akanipitisha karibu nayo pande zote; na tazama, palikuwa na mifupa mingi katika ule uwanda! Nayo, tazama, ilikuwa mikavu sana. Akaniambia, Mwanadamu, je! Mifupa hii yaweza kuishi? Nami nikajibu, Ee Bwana MUNGU, wajua wewe.”         

Mungu alipomuonyesha Ezekiel bonde lililokuwa limejaa mifupa ya wafu na iliyokuwa imekauka sana katika maono yale yeye hakujua kuwa uko uwezekano wa mifupa ile kufanywa hai, hivi ndivyo inavyokuwa wakati mwanadamu anapopitia mambo magumu na hivyo ndivyo ilivyokuwa katika moyo wa Yairo wakati akitarajia uponyaji wa binti yake anapokea taarifa kuwa asimsumbue Mwalimu (Rabbi) kwani binti yake amekwisha kufa, matumaini yake na ya wale waliomletea taarifa yalikuwa yametoweka na sasa kilichokuwa kinasubiriwa ni mipango ya mazishi ya binti wa miaka 12 akiwa anawaza hilo hata hivyo Yesu alikuwa anaona mambo kwa njia nyingine tofauti sana na mtazamo wa kawaida, alimtia moyo Yairio aamini tu asiogope na sio hivyo tu hata alipofika naye kwenye nyumba ya msiba na kuwakataza watu waache kelele za maombolezo kwani mtoto amelala tu wao walimcheka na kumdhihaki wakidhani labda huenda Yesu hajui hata maiti au mtu aliyekufa  

Marko 5:35-36. “Hata alipokuwa katika kunena, wakaja watu kutoka kwa yule mkuu wa sinagogi, wakisema, Binti yako amekwisha kufa; kwani kuzidi kumsumbua mwalimu?Lakini Yesu, alipolisikia lile neno likinenwa, akamwambia mkuu wa sinagogi, Usiogope, amini tu.”

Marko 5:38-39. “Wakafika nyumbani kwa yule mkuu wa sinagogi, akaona ghasia, na watu wakilia, wakifanya maombolezo makuu. Alipokwisha kuingia, akawaambia, Mbona mnafanya ghasia na kulia? Kijana hakufa, bali amelala tu.”

Je wewe unaona nini katika ndoto zako, unaona nini kazini kwako, unaona nini katika ndoa yako, uchumba wako, biashara zako, na maisha yako kwa ujumla, wakati unaona kuwa umefikia mwisho Mungu kwake yeye anaona ndio kwanza mwanzo unaanza, wakati wewe unaona giza yeye ndio kwanza kumekucha kile kinachoonekana kama mwisho kwako ni mapumziko ya muda tu, kamwe usikubali taarifa na tafasiri za watu ziwe tafasiri ya Mungu juu ya maisha yako! Mwangalie Yesu tu.

Kelele za watu hazibadilishi mpango wa Mungu

Walipofika nyumbani kwa Yairo kulikuwa na kelele, waombolezaji walikuwa wameshajaa tayari, na walilia kwa sauti kuu ya maombolezo na ngoma za maombolezo zilikuwa tayari zimeshawekwa  wakati wao wakifanya maombolezo kweli kweli Yesu alikuwa anaona wanafanya ghasia, na aliwakemea na kuwataka waache ghasia zao, wakati mwingine unapokuwa katika wakati mgumu watu wanaokuzunguka wanaweza kuongezea balaa katika majanga yaliyokupata kwani hata kama wewe ulikuwa na matumaini wao wanayafifisha zaidi, kila mmoja anajua kuwa mwisho wa maisha ya mwanadamu ni kifo na kila mtu anaelewa kuwa kifo ndio mwisho wa mambo yote na kwa sababu hiyo waliendelea na maombolezo na masikitiko na vilio ambavyo Yesu aliona kuwa wanafanya ghasia na alipowanyamazisha walimcheka sana, watu na mazingira yanayokuzunguka yanaweza kusema kuwa wewe uwezi tena, wanaweza kusema muda wako umeisha, wanaweza kusema hii ndio imetoka, Lakini Yesu ni kama alikuwa anamwambia Yairo usisikilize sauti za makelele na ghasia za watu wewe sikiliza sauti ya Yesu kelele za watu hazibadilishi mpango wa Mungu kamwe

Marko 5:38-43. “Wakafika nyumbani kwa yule mkuu wa sinagogi, akaona ghasia, na watu wakilia, wakifanya maombolezo makuu. Alipokwisha kuingia, akawaambia, Mbona mnafanya ghasia na kulia? Kijana hakufa, bali amelala tu. Wakamcheka sana. Naye alipokwisha kuwatoa nje wote, akamtwaa babaye yule kijana na mamaye, na wale walio pamoja naye, akaingia ndani alimokuwamo yule kijana. Akamshika mkono kijana, akamwambia, Talitha, kumi; tafsiri yake, Msichana, nakuambia, Inuka. Mara akasimama yule kijana, akaenda; maana alikuwa amepata umri wa miaka kumi na miwili. Mara wakashangaa mshangao mkuu. Akawaonya sana, mtu asijue habari ile; akaamuru apewe chakula.:”

Yesu alimshika mkono aliyekufa na akamwambia msichana nakuambia inuka, Yesu alitumia maeneno ya Kiaramu “Talitha kum” akimaanisha msichana amka, Yesu hakupiga makelele wala hakutaka kufanya muujiza huu kama maonyesho, alikuwa kazini kuwasaidia watu wenye uhitaji, alikuwa kazini kuahirisha msiba, alikuja kusaidia watu, yuko tayari kukusaidia na yuko tayari kukushika mkono, haijalishi moyo wako umepata ganzi kwa kiasi gani wala hijalishi umevunjika moyo kwa kiwango gani, haijalishi umefikia mwisho wa nguvu zako  yeye akikushika mkono uhai utakurudia wakati watu wanadhani imekwisha Yesu anasema inuka, hakuna hali yoyote ile isiyoweza kubadilishwa na Mungu, tumaini lako na ndoto zako haziwezi kuzikwa mbele za Yesu Krito wa Nazareth aliye hai, wakati watu wanafikiri kuwa hali yako itadumu Yesu anaiona hali yako ni ya muda tu kwa sababu hiyo usilie, wala suiogope, acha kutazama mazingira, wala hali yako wala kushindwa kwako kwa Yesu hakuna kitu kinakufa yeye anauwezo wa kuamsha na leo ataliamsha kwenye maisha yako kila jambo linaloonekana kuwa limekufa na watu wameanza kuzomea wakifikiri mwishi umefika, kwa Yesu Kesi yako sio mwisho, kwa Yesu amini tu usiogope kelele za watu hazibadilishi mpango wa Mungu

Mtoto hajafa amelala tu

Katika uwepo wa Mungu kifo ni jambo la muda na sio la milele, wala sio mwisho wa mambo, na ndio Maana Kristo katika mtazamo wake huona kifo kama usingizi tu, wakati wanadamu wanaona ndio mwisho wa kila kitu, Yesu anakiona kifo kama suingizi tu, sio tatizo kubwa yeye ndio huo ufufuo!

Yohana 11:11-14 “Aliyasema hayo; kisha, baada ya hayo, akawaambia, Rafiki yetu, Lazaro, amelala; lakini ninakwenda nipate kumwamsha.Basi wale wanafunzi wakamwambia, Bwana, ikiwa amelala, atapona.Lakini Yesu alikuwa amenena habari ya mauti yake; nao walidhania ya kuwa ananena habari ya kulala usingizi. Basi hapo Yesu akawaambia waziwazi, Lazaro amekufa.”

Yesu alikuwa akionyesha mamlaka yake kama mwana wa Mungu kuwa anao uwezo wa kufufua na ana mamlaka dhidi ya kifo, ni yeye ndiye anayeshikilia funguo (Mamlaka) ya kifo na uzima kwa hiyo yeye anauwezo wa kuwaamsha waliokufa kama anavyoamsha mtu usingizini, Mungu anatumia usemi huu kuwatia moyo wanadamu kuwa kile wanachokiona kama uzito kwake yeye ni chepesi kuliko wanavyofikiri, wanadamu wanapopoteza tumaini wakati wote wanapaswa wakumbuke kuwa yuko Mungu ambaye kwake mambo ni mepesi tu na ndio maana Yesu aliamua kuwatuliza waombolezaji  na kuwafukuzilia mbali na kuwaamuru kuacha ghasia, aidha Yesu alikuwa anataka kuficha mamlaka yake isijulikane na watu nguvu za Mungu sio kwaajili ya maonyesho bali ni kwaajili ya kuwasaidia watu wenye uhitaji, Yesu alikuwa amekuja kuahirisha msiba amkuja kuondoa ghasia

Yesu alichelewa wakati akiwa njiani kumhudumia mtoto wa Yairo ili kutoa muda wa kifo cha mtoto na habari za kifo ziweze kumfikia Yairo nan a majirani na ndugu na jamaa  pia waombolezaji wajikusanye na kufika  na kuanza kuomboleza, wataalamu wa kifo wathibitishe kuwa mtoto amekufa, mwili uoshwe na watu wasubiri amri ya mazishi kutoka kwa baba mzazi wa binti Yairo

Mathayo 9:23-26 “Yesu alipofika nyumbani kwa yule jumbe, aliona wapiga filimbi, na makutano wakifanya maombolezo, akawaambia, Ondokeni; kwa maana kijana hakufa, amelala tu. Wakamcheka sana. Lakini makutano walipoondoshwa, aliingia, akamshika mkono; yule kijana akasimama. Zikaenea habari hizi katika nchi ile yote.”

Mungu anapotaka kufanya mambo ya kushangaza huonekana kama amechelewa ili nguvu zake zionekane kwamba muda sio tatizo kwa Mungu, waombolezaji wakuzunguke ili jina la Mungu litukuzwe, wakati mwingine wambeya watapata habari ya yale yaliyokukuta na watasengenya na kusema Mungu atawaacha wazungumze kuwa jamaa amefikia mwisho  mambo yake yameharibika kwisha habaru yake hawezi kuinuka tena na kadhalika, kisha atafanya muujiza  na hapo kila mtu atajua kuwa Mungu ana uwezo anza kuchangamka ndugu yangu kwa sababu mtoto hajafa amelala tu, kinachokutokea ni kwaajili ya utukufu wa Mungu, yanakutokea ili majirani wapate taarifa, ili ndugu na jmaa wajue ili wasengenyaji wasema wakati wanakuza habari zako hapo anatikea mwanaume anaitwa Yesu anatangaza kuwa msifanye ghasia hapa mtoto hajafa amelala tu !

Yesu pia alkuwa akidhihirisha nguvu zake dhidi ya uumbaji kile anachokitamka ndicho kinachokuwa ni vizuri watu wakaamini katika neno la Mungu kuliko kuzitegemea akili zao wenyewe, Neno la Yesu lina nguvu kwa hiyo anapotamka kuwa ndoto zako hazijakufa zimelala tu ataamsha kila kinachoonekana kufa katika maisha yako, kwa uweza wake wa uumbaji, Yesu alimwamsha binti Yairo ataamsha kila kitu chako kinachoonekana kufa katika maisha yako  na watu wanakudhihaki watazuibwa vinywa vyao, anza kuchangamka kwa sababu mtoto hajafa amelala tu, anza kuzungumza lugha ya Bwana Yesu achana na lugha za waombolezaji hizo ni kelele tu mtoto hajafa amelala tu !

 [Korajabasta, para-kashata, roboboboso-kolotam katerrishetapapapa, kastabastariango, korabashandara-kasto, Yesukarabastanda-ding, koroposhotorabalistakarasto, taraka san sando pang-k-satostamanifesto, roborborboroshosta karabasa]

Mtoto hajafa amelala tu, kila kinachoonekana kufa katika maisha yako Katika jina la Yesu Kristo nakutamkia uzima naifukuza roho ya mauti naachilia uzima kila mahali katika mwili wako, katika ndoa yako, katika nyuimba yako,  katika familia yako, katika biashara yako, kazini kwako, katika afya yako nakutangazia uzima katika jina la Yesu Kristo mwana wa Mungu aliye hai amen! Mungu akutunze!

 

Rev. Innocent Samuel Kamote

Mkuu wa wajenzi mwenye hekima  

Jumapili, 22 Machi 2026

Yuaja mkuu wa ulimwengu huu, wala hana kitu kwangu!


Yohana 14:29-30 “Na sasa nimewaambia kabla halijatokea, kusudi litakapotokea mpate kuamini. Mimi sitasema nanyi maneno mengi tena, kwa maana yuaja mkuu wa ulimwengu huu, wala hana kitu kwangu.”



Utangulizi:

Ni muhimu kufahamu kuwa moja ya maswala ya msingi sana yaliyowahi kutamkwa na Yesu Kristo alipokuwa akiwaandaa wanafunzi wake kwaajili ya kusulubiwa kwake ni pamoja na maneno haya “Yuaja mkuu wa ulimwengu huu, wala hana kitu kwangu” maneno haya yalisemwa masaa machache kabla kidogo ya kukamatwa na maadui zake, kimsingi maneno hayo yalikuwa yanamuhusu Shetani na utendaji wake na kuhusika kwake moja kwa moja katika swala zima la kusulubiwa kwa Yesu Kristo, ambapo Yesu alikuwa akiliona tukio hilo hilo kua ni tukio la ushindi  la hiyari na kuwa ingawa shetani atahusika katika kukamatwa na kusulubiwa kwa Yesu Kristo, Yesu Kristo alikuwa na tafasiri nyingine kuwa litakuwa ni tukio la kuokolewa kwa watu wengi Duniani na ushindi wa kiroho.

Yohana 12:31-33 “Sasa hukumu ya ulimwengu huu ipo; sasa mkuu wa ulimwengu huu atatupwa nje. Nami nikiinuliwa juu ya nchi, nitawavuta wote kwangu. Aliyanena hayo akionyesha ni mauti gani atakayokufa.”

Yohana 13:26-27 “Basi Yesu akajibu, Ndiye mtu yule nitakayemtowelea tonge na kumpa. Akatowelea tonge, akalitwaa akampa Yuda, mwana wa Simoni Iskariote. Na baada ya hilo tonge Shetani alimwingia. Basi Yesu akamwambia, Uyatendayo yatende upesi.”

Njama, mipango na usaliti pamoja na swala zima la kukamatwa kwa Yesu na mpango mzima wa kuteswa kwake na kusulubiwa msalabani kwa namna Fulani kulionekana kama kufaulu kwa mbinu za ibilisi kwani kuliratibiwa chini ya uwepo wa shetani, hata hivyo Yesu anatufungua katika kifungu hiki cha msingi kuwa mpango huo hauna madhara kwake na kuwa ni ushindi wa kiroho wa hali ya juu. Ni kwa msingi huo basi leo tutachukua muda kutafakari kwa pamoja somo hili muhimu Yuaja mkuu wa ulimwengu huu, wala hana kitu kwangu!, tutajifunza somo hili kwa kuzingatia vipengele muhimu vitatu vifuatavyo:-

·         Maana ya neno mkuu wa ulimwengu huu.

·         Yuaja mkuu wa ulimwengu huu.

·         Wala hana kitu kwangu.

Maana ya neno mkuu wa ulimwengu huu.

Yohana 14:29-30 “Na sasa nimewaambia kabla halijatokea, kusudi litakapotokea mpate kuamini. Mimi sitasema nanyi maneno mengi tena, kwa maana yuaja mkuu wa ulimwengu huu, wala hana kitu kwangu.”

Yesu Kristo aliyazungumza maneno hayo muda mfupi kidogo kabla ya kukamatwa kwake na kusulubiwa msalabani kwa mateso mabaya sana, maneno yake hayo yanatufunulia siri nzito kuhusu ushindi utakaoambatana na mateso yake, ushindi unaotokana na kuzizidi hila za shetani na njama zake; Maneno anayoyatumia hapo Mkuu wa ulimwengu huu yana maana gani hasa? Kimsingi neno yuaja mkuu wa ulimwengu huu wala hana kitu kwangu yanasomeka hivi katika lugha ya Kiyunani ona  “yáp archon toutou kósmos erchomai, kai echo oύ oudeis en emoi”  na katika kiingereza cha KJV ambayo ni literal translation Bible yaani ni biblia iliyotafasiriwa kwa mtindo wa neno kwa neno andiko hilo linasomeka hivi  “for the Prince of this world cometh, and hath nothing in me”  NIV yenyewe ambayo ni dynamic translation  inasomeka hivi “for the prince of this world is coming, He has no hold on me” kwa hiyo utabaini kuwa neno Mkuu wa ulimwengu huu au Prince of this world katika Kiyunani anaitwa “Archon” ambalo maana yeke hasa kwa Kiingereza ni “a person in authority” au “a magistrate” kimsingi Yesu alikuwa akimtaja shetani hapo ambaye anatajwa kama mwendesha mashitaka na ushawishi katika mfumo wa ulimwengu huu wa uovu “Ksómos”  taratibu zote za uovu za dunia zinaendeshwa na shetani kwa hiyo kutokana na kazi zake hizo anaitwa mtawala wa dunia hii, au mungu wa dunia hii au mkuu wa anga anayetamalaki falme na mamlaka za kiovu duniani.

Waefeso 2:1-3 “Nanyi mlikuwa wafu kwa sababu ya makosa na dhambi zenu; ambazo mliziendea zamani kwa kuifuata kawaida ya ulimwengu huu, na kwa kumfuata mfalme wa uwezo wa anga, roho yule atendaye kazi sasa katika wana wa kuasi; ambao zamani, sisi sote nasi tulienenda kati yao, katika tamaa za miili yetu, tulipoyatimiza mapenzi ya mwili na ya nia, tukawa kwa tabia yetu watoto wa hasira kama na hao wengine.”

Waefeso 6:10-12 “Hatimaye, mzidi kuwa hodari katika Bwana na katika uweza wa nguvu zake. Vaeni silaha zote za Mungu, mpate kuweza kuzipinga hila za Shetani. Kwa maana kushindana kwetu sisi si juu ya damu na nyama; bali ni juu ya falme na mamlaka, juu ya wakuu wa giza hili, juu ya majeshi ya pepo wabaya katika ulimwengu wa roho.”

Ulimwengu wa uovu uko chini ya utawala na ushawishi na uendeshaji wa kishetani, changamoto na mapambano anayokutana nayo mwanadamu yanayopingana na maisha yetu ya kila siku na mafanikio yetu na uonevu ni matokeo ya kimwili ya kushindana kwetu katika ulimwengu wa kiroho wa utendaji wa shetani ambaye pia huitwa Mungu wa dunia hii.

2Wakorintho 4:3-4 “Lakini ikiwa injili yetu imesitirika, imesitirika kwa hao wanaopotea; ambao ndani yao mungu wa dunia hii amepofusha fikira zao wasioamini, isiwazukie nuru ya injili ya utukufu wake Kristo aliye sura yake Mungu.”

Kwa hiyo Yesu anayasema mambo hayo akiwaonyesha wanafunzi wake kuwa saa yake imewadia ya kwenda kupambana na mkuu wa ulimwengu huu, ni wakati wake sasa kwenda kufanya kazi ambayo kwa akili zake mawazo yake na mpango wake ni kuwa anakwenda kummaliza Yesu Kristo lakini Yesu Kristo katika hekima yake na mpango wake anaonyesha kuwa mpango na mkakati mzima wa ibilisi hautakuwa na mashiko kwake! 

Yuaja mkuu wa ulimwengu huu.

Kwa nini Yesu anatumia neno yuaja? Shetani alikuwa wapi na kwanini Yuaja? Neno yuaja katika Biblia ya kiyunani hapo kama tulivyoona linatumika neno “erchomai” ambalo kwa kiingereza ni “to come” au “to go” ambalo hasa linatumika kuelezea ujio halisi katika mwili  “a Physical movement” kama alikuwa akizunguka zunguka huko na kule katika ulimwengu wa roho sasa anakuja akiwa amejikamilisha kwa hiyo anakuja akijitokeza hadharani “to appear in public” “a physical arrival” kwa hiyo Shetani alikuwa amewapagaa rasmi Yuda, Viongozi wa dini, mahakama na askari wanakuja rasmi sasa kuendesha mateso na kufanya kazi ya kuua kupitia kusulubiwa kikatili, ni muhimu kuelewa hapo kuwa shetani anapokuja wazi kama alivyokuja wakati wa kumkamata Yesu maana yake ni wakati anapowavaa watu na watu hao sasa wanakuwa hawana huruma wanaingiwa na roho ya kikatili, roho mbaya inawakalia huruma ya kibinadamu inaondoka sasa wanakukusudia mabaya, kuharibu kusambaratisha na kuua!

1Petro 5:8-9 “Mwe na kiasi na kukesha; kwa kuwa mshitaki wenu Ibilisi, kama simba angurumaye, huzunguka-zunguka, akitafuta mtu ammeze. Nanyi mpingeni huyo, mkiwa thabiti katika imani, mkijua ya kuwa mateso yale yale yanatimizwa kwa ndugu zenu walioko duniani.”

Ayubu 2:7-8 “Basi Shetani akatoka mbele za uso wa Bwana, akampiga Ayubu na majipu mabaya tangu wayo wa mguu hata utosi wa kichwa. Naye akashika kigae cha kujikunia; akaketi majivuni.”

Yohana 10:10-11 “Mwivi haji ila aibe na kuchinja na kuharibu; mimi nalikuja ili wawe na uzima, kisha wawe nao tele.Mimi ndimi mchungaji mwema. Mchungaji mwema huutoa uhai wake kwa ajili ya kondoo.”

Shetani anapokuja wazi wazi madhara yake yanaonekana wazi wazi, uharibifu mkubwa hutokea, wizi wa Afya mali na uvunjifu mkubwa wa maadili, mafarakano, ukatili uliopitiliza, anapokuja huwa anachinja ni tofauti na Yesu anapokuja, wakati Yesu anapokuja anaokoa, anakuja na uzima wa milele, shetani anapokuja anakuja na kufukuzwa kazi, anakuja na talaka, anakuja na uvamizi, anakuja kuleta hali mbaya, analeta usaliti, analeta mafarakano, kutokuelewana, anakuja na majungu, anakuja na matukio ya kuhuzunisha, hasara, na uhaini, mateso, dharau, matukano na kadhalika  hapo unapoona mambo mabaya yanakuandama kila kitu hakiendi ni kama una nuksi, mikosi na balaa ujue amekuja, Shetani anapokuja maana yake anakuja na kufikia kilele  cha utendaji wa kazi yake katika maisha yetu ataharibu kwa kiasi ambacho unaweza kufikiri kuwa Mungu hana huruma, utashuhudia utendaji wake wa kikatili ambao huwezi kulinganisha na siku au wakati mwingine wowote katika maisha.

Wala hana kitu kwangu.

Yohana 14:29-30 “Na sasa nimewaambia kabla halijatokea, kusudi litakapotokea mpate kuamini. Mimi sitasema nanyi maneno mengi tena, kwa maana yuaja mkuu wa ulimwengu huu, wala hana kitu kwangu.”

Haleluya, habari njema ni kuwa Yesu alitoa taarifa hizo Yuaja mkuu wa ulimwengu huu lakini aliwathibitishia wanafunzi wake kuwa vyo vyote iwavyo hata kama anakuja na saa ile anayokuja inaonekana kuwa ni ya kutisha sana huyu jamaa hana kitu kwake!  Neno wala hana kitu kwangu linasomeka katika Kiyunani “kai echo oύ oudeis en emoi”  kwa kiingereza ESV as “No claim on me” NIV “nothing in me” NASB “ No power over me” KJV “and hath nothing in me” maana yake ni nini hasa anachokimaanisha Yesu ni kuwa pamoja na ujio wake huu wenye hatari wa kumsulubisha mwana wa Mungu Shetani hana udhibiti wowote juu ya Yesu, hana uhalali wowote, hana mamlaka yoyote, wala hausiki kwa lolote wala hana sehemu katika mpango wa Mungu wa ukombozi wa mwanadamu kupitia mauti ya Yesu msalabani Yesu haendi msalabani kwa sababu ya dhambi zake au makosa yake  anaenda kwa mpango wa Mungu kwa hiyari yake mwenyewe, kwani uwezo wa kuutoa uhai anao na uwezo wa kuutwaa anao, hakuna wa kumshitaki Yesu Kristo, uwezo huo uko kwenye mamlaka ya kimbinguni, na sio shetani wala serikali wala makuhani

Yohana 10:17-18 “Ndiposa Baba anipenda, kwa sababu nautoa uhai wangu ili niutwae tena. Hakuna mtu aniondoleaye, bali mimi nautoa mwenyewe. Nami ninao uweza wa kuutoa, ninao na uweza wa kuutwaa tena. Agizo hilo nalilipokea kwa Baba yangu.”

Yohana 19:10-11. “Basi Pilato akamwambia, Husemi nami? Hujui ya kuwa mimi nina mamlaka ya kukufungua, nami nina mamlaka ya kukusulibisha? Yesu akamjibu, Wewe hungekuwa na mamlaka yo yote juu yangu, kama usingepewa kutoka juu; kwa hiyo yeye aliyenitia mikononi mwako yuna dhambi iliyo kubwa zaidi.”

Yohana 8:46-47 “Ni nani miongoni mwenu anishuhudiaye ya kuwa nina dhambi? Nami nikisema kweli, mbona ninyi hamnisadiki? Yeye aliye wa Mungu huyasikia maneno ya Mungu; hivyo ninyi hamsikii kwa sababu ninyi si wa Mungu.”

Waebrania 4:14-15 “Basi, iwapo tunaye kuhani mkuu aliyeingia katika mbingu, Yesu, Mwana wa Mungu, na tuyashike sana maungamo yetu.Kwa kuwa hamna kuhani mkuu asiyeweza kuchukuana nasi katika mambo yetu ya udhaifu; bali yeye alijaribiwa sawasawa na sisi katika mambo yote, bila kufanya dhambi.”

Kitendo cha Yesu kusulubiwa na kufa msalabani kwa mateso makali, hakikutokana na uwezo wa shetani bali ulikuwa ni mpango wa Mungu wa ukombozi wa mwanadamu, kimsingi shetani alihusika kwa upumbavu wake akiwatumia viongozi wa dunia hii waliopagawa na fikra zake, Lakini wakati anajihusisha katika mpango huu alijikaanga kabisa

1Wakorintho 2:6-9 “Walakini iko hekima tusemayo kati ya wakamilifu; ila si hekima ya dunia hii, wala ya hao wanaoitawala dunia hii, wanaobatilika; bali twanena hekima ya Mungu katika siri, ile hekima iliyofichwa, ambayo Mungu aliiazimu tangu milele, kwa utukufu wetu; ambayo wenye kuitawala dunia hii hawaijui hata mmoja; maana kama wangaliijua, wasingalimsulibisha Bwana wa utukufu; lakini, kama ilivyoandikwa, Mambo ambayo jicho halikuyaona wala sikio halikuyasikia, (Wala hayakuingia katika moyo wa mwanadamu,) Mambo ambayo Mungu aliwaandalia wampendao.”

Isaya 53:3-5 “Alidharauliwa na kukataliwa na watu; Mtu wa huzuni nyingi, ajuaye sikitiko; Na kama mtu ambaye watu humficha nyuso zao, Alidharauliwa wala hatukumhesabu kuwa kitu. Hakika ameyachukua masikitiko yetu, Amejitwika huzuni zetu; Lakini tulimdhania ya kuwa amepigwa, Amepigwa na Mungu, na kuteswa. Bali alijeruhiwa kwa makosa yetu, Alichubuliwa kwa maovu yetu; Adhabu ya amani yetu ilikuwa juu yake, Na kwa kupigwa kwake sisi tumepona.”

Yesu alitaka tuelewe ya kuwa vita katika ulimwengu wa roho ni halisi, shetani yuko nyuma ya kila linalokupata anatumia usaliti, mateso na chuki lakini hata hivyo hana kitu kwa Yesu Kristo, sio tu kwa Yesu Kristo bali na kwa kila aaminiye kila mtu anayemkubali Yesu Kristo hapa duniani au ulimwenguni anakuwa kama Yesu kwa hiyo kama yeye alivyo ndivyo tulivyo, kwa hiyo kila yajapo mateso na dhiki za aina yoyote tunajua kuwa amekuja mkuu wa ulimwengu huu lakini hana kitu kwangu, zikija dhiki hivyo hivyo yakija magonjwa wewe jua yanakuja tu lakini hayana kitu kwako kwa sababu wewe ni kama alivyokuwa Kristo hapa duniani una Mungu aliye hai ndani yako

1Yohana 4:15-17 “Kila akiriye ya kuwa Yesu ni Mwana wa Mungu, Mungu hukaa ndani yake, naye ndani ya Mungu. Nasi tumelifahamu pendo alilo nalo Mungu kwetu sisi, na kuliamini. Mungu ni upendo, naye akaaye katika pendo, hukaa ndani ya Mungu, na Mungu hukaa ndani yake. Katika hili pendo limekamilishwa kwetu, ili tuwe na ujasiri katika siku ya hukumu; kwa kuwa, kama yeye alivyo, ndivyo tulivyo na sisi ulimwenguni humu.”

1Yohana 4:4 “Ninyi, watoto wadogo, mwatokana na Mungu nanyi mmewashinda, kwa sababu yeye aliye ndani yenu ni mkuu kuliko yeye aliye katika dunia.”  

Ni kutokana na ushindi aliotupa Yesu Kristo pale msalabani una haki ya kumuambia shetani, magonjwa, dhiki, shida, changamoto kuwa najua umekuja lakini huna kitu kwangu, wachawi hawana madhara kwako, wambeya hawana madhara kwako, wafitini hawana madhara kwako chochote kinachokukabili hapa duniani fahamu amekuja tu lakini hana kitu kwako tembea katika ushindi huu tangu sasa tambua ya kuwa Yesu amekutetea amekufanya kuwa mshindi wa changamoto zozote zinazoendelea hapa duniani usikate tamaa wala usilie unapoteseka wala usimlaani Mungu na kumlaumu na kumuona kama amekuacha wewe tambua tu kuwa kama una Yesu kama una Mungu aliye ndani yako ni mkuu kuliko aliye katika dunia hii sema kila wakati na sema na kila changamoto ya kuwa najua kuwa yu aja mkuu wa ulimwengu huu kwa vyovyote vile hana kitu kwangu katika jina la Yesu Kristo kumbe kama alivyokuwa Yesu hapa ulimwenguni ndivyo tulivyo kwa sababu hiyi shetani hana kitu kwako na kwangu katika jina la Yesu Mwana wa Mungu aliye hai  ameen !        

Na. Rev. Innocent Samuel Kamote

Mkuu wa wajenzi mwenye Hekima