Jumatatu, 25 Mei 2026

Yawafaa ninyi Mimi niondoke!

 


Yohana 16:7-13 “Lakini mimi nawaambia iliyo kweli; yawafaa ninyi mimi niondoke, kwa maana mimi nisipoondoka, huyo Msaidizi hatakuja kwenu; bali mimi nikienda zangu, nitampeleka kwenu. Naye akiisha kuja, huyo atauhakikisha ulimwengu kwa habari ya dhambi, na haki, na hukumu. Kwa habari ya dhambi, kwa sababu hawaniamini mimi; kwa habari ya haki, kwa sababu mimi naenda zangu kwa Baba, wala hamnioni tena; kwa habari ya hukumu, kwa sababu yule mkuu wa ulimwengu huu amekwisha kuhukumiwa. Hata bado nikali ninayo mengi ya kuwaambia, lakini hamwezi kuyastahimili hivi sasa. Lakini yeye atakapokuja, huyo Roho wa kweli, atawaongoza awatie kwenye kweli yote; kwa maana hatanena kwa shauri lake mwenyewe, lakini yote atakayoyasikia atayanena, na mambo yajayo atawapasha habari yake.”



Utangulizi:

Ni muhimu kufahamu kuwa Yesu Kristo alikuwa anazungumza maneno haya mwishoni kabisa mwa huduma yake akiwa amewaaga wanafunzi wake ya kuwa yeye ameikamilisha kazi aliyotumwa kuifanya na kuwa anarudi kwa Baba, Yesu alikuwa amewaeleza wanafunzi wake kuwa atasulubiwa, kufa na kufufuka, na kuikamilisha kazi ya ukombozi wa mwanadamu, na baada yake nini kingelifuata. Yesu anaonyesha kwa uwazi umuhimu wa kuja kwa Roho Mtakatifu, hili lilikuwa ni jambo la muhimu sana kwani lingeondoa hofu ya wanafunzi wake na kuifanya kazi ya Mungu kupanuka kwa kina zaidi na hivyo kuondoka kwake kulikuwa na faida zaidi kuliko hasara ambayo wanafunzi wake walikuwa wakiifikiria, Yesu alikuwa anafahamu changamoto ambazo zingewakabili wanafunzi wake baada yake na hivyo alitaka kuwathibitishia kuwa uwepo wa Roho Mtakatifu utakuwa na umuhimu zaidi na suluhu kwa hofu yao

Yohana 14:16-17 “Nami nitamwomba Baba, naye atawapa Msaidizi mwingine, ili akae nanyi hata milele; ndiye Roho wa kweli; ambaye ulimwengu hauwezi kumpokea, kwa kuwa haumwoni wala haumtambui; bali ninyi mnamtambua, maana anakaa kwenu, naye atakuwa ndani yenu.”

Kimsingi Yesu Kristo alilizungumzia swala na ujio wa Roho Mtakatifu kama swala muhimu sana  na hitaji la msingi katika maisha ya kiroho ya  wanafunzi wake na kila aaminiye  baadaye na huduma, Yesu alitaka wanafunzi wake wawe na uelewa mpana kuhusu umuhimu wa Roho Mtakatifu na kuonyesha wazi kuwa hatuwezi kwa namna yoyote ile kuishi duniani na kutimiza kusudi la Mungu bila msaada wa Roho Mtakatifu na nguvu zake mwenyewe, kwa msingi huo katika msimu huu wa juma la Pentekoste tutachukua  muda kutafakari kwa kina na mapana  na marefu umuhimu wa Roho Mtakatifu katika maisha yetu, na kujumuika kwa pamoja katika maombezi ya ubatizo wa Roho Mtakatifu na  hivyo tutajifunza somo hili “Yawafaa ninyi mimi niondoke” kwa kuzingatia vipengele vitatu vifuatavyo:

·         Yawafaa ninyi mimi niondoke

·         Kazi za Roho Mtakatifu Duniani

·         Ubatizo wa Roho Mtakatifu

Yawafaa ninyi mimi niondoke!

Kimsingi Roho Mtakatifu ametolewa na Mungu Baba yetu ili akae nasi milele na kuikamilisha ile kazi iliyoanzishwa na Yesu Kristo hapa duniani, Yesu alikuwa hana budi kuteswa na kufa msalabani kisha kufufuka siku ya tatu na kupaa kwenda mbinguni mpaka wakati ulioamriwa, Ujio wa Roho Mtakatifu ulikuwa ni wa Muhimu sana kwa sababu kuweko wa Yesu Duniani katika mwili wa kibinadamu kulimpa mipaka ya kihuduma na alilazimika kuweko mahali pamoja kwa wakati mmoja lakini kwa kitendo cha kupaa na kurudi kwa Baba angetoa ruhusa kwa Roho Mtakatifu kuja na kukaa na sisi daima  na kuuleta uwepo wa Mungu kwa kila mmoja kokote aliko Duniani, Kutokana na umuhimu wa Roho Mtakatifu, Yesu aliwaagiza wanafunzi wake kutokuianza kazi ya Mungu kwanza mpaka wamepokea ubatizo wa Roho Mtakatifu ambaye angewageuza,  kuwapa nguvu na kuwafanya kuwa mashahidi wake

Matendo 1:4-8 “Hata alipokuwa amekutana nao aliwaagiza wasitoke Yerusalemu, bali waingoje ahadi ya Baba, ambayo mlisikia habari zake kwangu; ya kwamba Yohana alibatiza kwa maji, bali ninyi mtabatizwa katika Roho Mtakatifu baada ya siku hizi chache. Basi walipokutanika, wakamwuliza, wakisema, Je! Bwana, wakati huu ndipo unapowarudishia Israeli ufalme? Akawaambia, Si kazi yenu kujua nyakati wala majira, Baba aliyoyaweka katika mamlaka yake mwenyewe. Lakini mtapokea nguvu, akiisha kuwajilia juu yenu Roho Mtakatifu; nanyi mtakuwa mashahidi wangu katika Yerusalemu, na katika Uyahudi wote, na Samaria, na hata mwisho wa nchi.”

Luka 24:46-49 “Akawaambia, Ndivyo ilivyoandikwa, kwamba Kristo atateswa na kufufuka siku ya tatu; na kwamba mataifa yote watahubiriwa kwa jina lake habari ya toba na ondoleo la dhambi, kuanza tangu Yerusalemu. Nanyi ndinyi mashahidi wa mambo haya. Na tazama, nawaletea juu yenu ahadi ya Baba yangu; lakini kaeni humu mjini, hata mvikwe uwezo utokao juu.”

Wanafunzi wa Yesu Kristo walikuwa pamoja naye kwa zaidi ya miaka mitatu na nusu, wakijifunza maarifa elimu na uwezo wa kufanya huduma lakini pamoja na yote haya Yesu anawaamuru wasitoke kufanya lolote mpaka wapokee ahadi ya Baba, hii ilikuwa na maana iliyo wazi ya kuwa Elimu, ujuzi na maarifa pekee hautoshi, uzoefu hautoshi, vipawa vya kibinadamu havitoshi ili tuwe wanafunzi wa Yesu waliokamilika tunamuhitaji sana Roho Mtakatifu. Uwepo wa Roho Mtakatifu ambaye haonekani kwa macho katika maisha ya wanafunzi wa Yesu ni wa muhimu zaidi kuliko uwepo wa Yesu katika hali ya mwili, Roho Mtakatifu asingeliweza kuja kama Yesu angeendelea kubaki, Kupaa kwa Yesu Kristo, na kutukuzwa kwake mbinguni kungeruhusu ujio wa Roho Mtakatifu ambaye uwepo wake ungesababisha uwepo wa Mungu kukaa ndani ya kila mwamini kokote aliko duniani, lakini pia kazi ya kutukuzwa kwa Yesu Kristo Duniani  ingeanza kupitia Roho Mtakatifu sawasawa na jinsi ambavyo Yesu ametukuzwa Mbinguni.

Kazi za Roho Mtakatifu Duniani

-          Roho Mtakatifu ni Msaidizi mwingine – Yesu Kristo alikuwa anafahamu kuwa Wanafunzi wake wangekabiliwa na changamoto kali  na kubwa na upinzani mkali wa aina mbalimbali na wangekata tamaa hasa baada ya kuondoka kwake, Yeye alipokuwa pamoja nao alikuwa ni mtetezi mkubwa sana wa wanafunzi wake na mashambulizi yote ya adui yalielekezwa kwake, Kuondoka kwake Yesu Kristo ilikuwa sababu ya huzuni nyingi sana hofu na mashaka na walikata tamaa, Yesu aliwaahidi kuwa atawaletea msaidizi mwingine

 

Yohana 14:16-17 “Nami nitamwomba Baba, naye atawapa Msaidizi mwingine, ili akae nanyi hata milele; ndiye Roho wa kweli; ambaye ulimwengu hauwezi kumpokea, kwa kuwa haumwoni wala haumtambui; bali ninyi mnamtambua, maana anakaa kwenu, naye atakuwa ndani yenu.”

 

Neno Msaidizi mwingine katika lugha ya kiyunani (Koine Greek) linasomeka kama “Paraklētos” ambalo maana yake Msaidizi, mtetezi, mfariji, mshauri au mtu anayesimama karibu na wewe kwa kusudi la kukutetea wakili (Advocate) Kazi hii inafanywa na Roho Mtakatifu kwa kila mtu aliyemuamini hata leo, kwa sababu hiyo kila mtu aliyeokoka anamuhitaji yeye kama uwepo wa Mungu katika maisha yetu ya kila siku.

 

-          Roho Mtakatifu anauwezo wa kubadilisha maisha – Wanafunzi wa Yesu Kristo walikuwa wanahitaji mabadiliko makubwa ya maisha yao, wengine walikuwa waoga, wasiojiamini, wenye ukali, wenye kisasi, wasioweza kusamehe na walihitaji mabadiliko makubwa sana, Roho Mtakatifu ndiye njia inayohusika katika mfumo mzima wa kubadili maisha ya mtu na kumfanya afae kwa kazi ile ambayo Mungu anaihiitahi katika maisha, ni pale tu Roho wa Mungu anapokuwa juu ya mtu kwa ubatizo ndipo anapoweza kubadilisha maisha ya mtu huyo na kumfanya afae kwa matumizi ya kazi ya ufalme wa Mungu.

 

1Samuel 10:5-7 “Baada ya hayo utafika Gibea ya Mungu, hapo palipo na ngome ya Wafilisti; kisha itakuwa, utakapofika mjini, utakutana na kundi la manabii wakishuka kutoka mahali pa juu, wenye kinanda, na tari, na kinubi, na filimbi mbele yao, nao watakuwa wakitabiri; na roho ya Bwana itakujilia kwa nguvu, nawe utatabiri pamoja nao, nawe utageuzwa kuwa mtu mwingine. Basi, hapo ishara hizi zitakapokutukia, fanya kama uonavyo vema; kwa kuwa Mungu yu pamoja nawe.”

 

Wagalatia 5:16-25 “Basi nasema, Enendeni kwa Roho, wala hamtazitimiza kamwe tamaa za mwili. Kwa sababu mwili hutamani ukishindana na Roho, na Roho kushindana na mwili; kwa maana hizi zimepingana, hata hamwezi kufanya mnayotaka. Lakini mkiongozwa na Roho, hampo chini ya sheria. Basi matendo ya mwili ni dhahiri, ndiyo haya, uasherati, uchafu, ufisadi, ibada ya sanamu, uchawi, uadui, ugomvi, wivu, hasira, fitina, faraka, uzushi,husuda, ulevi, ulafi, na mambo yanayofanana na hayo, katika hayo nawaambia mapema, kama nilivyokwisha kuwaambia, ya kwamba watu watendao mambo ya jinsi hiyo hawataurithi ufalme wa Mungu.Lakini tunda la Roho ni upendo, furaha, amani, uvumilivu, utu wema, fadhili, uaminifu, upole, kiasi; juu ya mambo kama hayo hakuna sheria. Na hao walio wa Kristo Yesu wameusulibisha mwili pamoja na mawazo yake mabaya na tamaa zake.Tukiishi kwa Roho, na tuenende kwa Roho.”

 

Ubatizo wa Roho Mtakatifu unatubadilisha maisha na kutufanya au kutusaidia kuishi maisha matakatifu siku hadi siku, kutembea katika Roho Mtakatifu kutayafanya maisha yetu yaachane na zile hali za mwili na kuruhusu ukomavu na kuzaliwa kwa matunda ya Roho Mtakatifu katika maisha yetu na kumlingania Yesu.

 

-          Roho Mtakatifu hutuvika uwezo au Nguvu kutoka juu – Kuihubiri injili na kuishi maisha ya ushuhuda kunahitaji nguvu za Mungu, Mungu anapowatuma watu katika ulimwengu huu anawavika nguvu kwa sababu kuna nguvu za upinzani ambazo tutakabiliana nazo duniani nguvu hii  tunayovikwa na Roho wa Mungu katika lugha ya kitaalamu ya maandiko ya agano jipya inaitwa “Dunamis” hili ni neno la Kiyunani (Koine Greek) ambalo lina maanisha uwezo, nguvu za Mungu, Nguvu zenye matokeo na mamlaka, nguvu hii husaidia waamini kukabiliana na upinzani wa anaina yoyote na kuwa tayari hata kufa kwaajili ya jina la Bwana na kwaajili ya ufalme wa Mungu, Wale waliokuwa na hofu na woga waliweza kutiwa nguvu na kuwa majasiri mara baada ya kubatizwa katika Roho Mtakatifu, tutakuwa na uwezo wa kukabiliana na upinzani wa aina yoyote na kuwa tayari hata kufa kwaajili ya jina la Bwana kama tutabatizwa kwa Roho Mtakatifu.

 

Luka 24:46-49 “Akawaambia, Ndivyo ilivyoandikwa, kwamba Kristo atateswa na kufufuka siku ya tatu; na kwamba mataifa yote watahubiriwa kwa jina lake habari ya toba na ondoleo la dhambi, kuanza tangu Yerusalemu. Nanyi ndinyi mashahidi wa mambo haya. Na tazama, nawaletea juu yenu ahadi ya Baba yangu; lakini kaeni humu mjini, hata mvikwe uwezo utokao juu.”

 

Matendo 1:8 “Lakini mtapokea nguvu, akiisha kuwajilia juu yenu Roho Mtakatifu; nanyi mtakuwa mashahidi wangu katika Yerusalemu, na katika Uyahudi wote, na Samaria, na hata mwisho wa nchi.”

 

-          Roho Mtakatifu atatuongoza katika kweli yote – Kweli yote ya Mungu haiwezi kueleweka kwa akili za kawaida peke yake, Lakini Roho Mtakatifu ni Mwalimu, yeye ni mwandishi wa neno la Mungu, ni Mwalimu na anaweza kutupa ufunuo wa kweli,  lakini sio hivyo tu Roho Mtakatifu atatukumbusha katika maswala yote muhimu na ya msingi katika mafundisho ya Yesu Kristo, Yeye hufanya kazi ya kutufunulia maswala yote kuhusu Mungu na mapenzi yake, Katika ulimwengu huu kila mtu anadai anayo kweli lakini ni kazi ya Roho Mtakatifu ambaye anaitwa Roho wa kweli kuufunua ukweli halisi sawasawa na ufunuo wa neno la Mungu.

 

Yohana 14:26 “  Lakini huyo Msaidizi, huyo Roho Mtakatifu, ambaye Baba atampeleka kwa jina langu, atawafundisha yote, na kuwakumbusha yote niliyowaambia.”

 

1Wakorintho 2:10-14 “Lakini Mungu ametufunulia sisi kwa Roho. Maana Roho Huchunguza yote, hata mafumbo ya Mungu, Maana Ni nani katika binadamu ayajuaye mambo ya binadamu ila roho ya binadamu iliyo ndani yake? Vivyo hivyo na mambo ya Mungu hakuna ayafahamuye ila Roho wa Mungu. Lakini sisi hatukuipokea roho ya dunia, bali Roho atokaye kwa Mungu, makusudi tupate kuyajua tuliyokirimiwa na Mungu.  Nayo twayanena, si kwa maneno yanayofundishwa kwa hekima ya kibinadamu, bali yanayofundishwa na Roho, tukiyafasiri mambo ya rohoni kwa maneno ya rohoni. Basi mwanadamu wa tabia ya asili hayapokei mambo ya Roho wa Mungu; maana kwake huyo ni upuzi, wala hawezi kuyafahamu, kwa kuwa yatambulikana kwa jinsi ya rohoni.”

 

-          Roho Mtakatifu humshuhudia Yesu Kristo – Kumshuhudia Yesu Kristo katika lugha ya asili ya kiyunani linatumika neno “martureō ambalo kwa kiingereza ni sawa na  neno “giving evidence”, au “well report about me”, maana yake ni kuwa Roho Mtakatifu atathibitisha ukweli kuhusu Yesu Kristo ni nani au ataelezea vizuri kuhusu Yesu Kristo, ana ushahidi wa kina kuhusu Yesu Kristo, kwa hiyo kama Mwalimu wa kweli atawaelekeza watu kumjua Yesu Kristo kwa kina zaidi ya alivyojulikana kwa wakati ule, na anavyoelezewa katika maandiko, atamuinua Yesu Kristo atathibitisha mafundisho yake kwa hiyo huduma yoyote ya kiroho au inayoongozwa kiroho haitakuwa na malengo ya kumuinua mtu bali itakuwa inamuinua Yesu Kristo, huduma yoyote ambayo haimuinui Yesu Kristo inahitaji kupimwa , na mtumishi yoyote ambaye hamuinui Yesu hatuna budi kumwangalia kwa makini na nabii yeyote ambaye anajitukuza yeye kuliko Kristo naye ni wa kuangaliwa kwa makini, ukiona imani yoyote inamuinua yeyote zaidi ya Kristo basi ni imani yenye mashaka.

 

Yohana 15:26 “Lakini ajapo huyo Msaidizi, nitakayewapelekea kutoka kwa Baba, huyo Roho wa kweli atokaye kwa Baba, yeye atanishuhudia.”

 

1Wakorintho 12:3Kwa hiyo nawaarifu, ya kwamba hakuna mtu anenaye katika Roho wa Mungu, kusema, Yesu amelaaniwa; wala hawezi mtu kusema, Yesu ni Bwana, isipokuwa katika Roho Mtakatifu.”

-          Roho Mtakatifu hutoa nyenzo za kutendea kazi – Ziko nyenzo za kutendea kazi ya Mungu ambazo hutolewa na Roho Mtakatifu ni maarufu sana kama karama za Roho Mtakatifu, hizi husaidia kurahisisha kazi ya Mungu na kulithibitisha neno na kuufaidia mwili wa Kristo, bila karama na utendaji wa Roho Mtakatifu kupitia karama hizo maneno yetu yatakuwa ni maneno yasiyo na uthibitisho au yanaweza kuwa kama hekima tu za wanadamu (Yaani Falsafa) au maneno ya kushawishi, lakini litakuwa ni neno lenye kuthibitishwa

 

1Wakorintho 2:4-5 “Na neno langu na kuhubiri kwangu hakukuwa kwa maneno ya hekima yenye kushawishi akili za watu, bali kwa dalili za Roho na za nguvu, ili imani yenu isiwe katika hekima ya wanadamu, bali katika nguvu za Mungu.”

 

1Wakorintho 12:7-11 “Lakini kila mmoja hupewa ufunuo wa Roho kwa kufaidiana. Maana mtu mmoja kwa Roho apewa neno la hekima; na mwingine neno la maarifa, apendavyo Roho yeye yule; mwingine imani katika Roho yeye yule; na mwingine karama za kuponya katika Roho yule mmoja; na mwingine matendo ya miujiza; na mwingine unabii; na mwingine kupambanua roho; mwingine aina za lugha; na mwingine tafsiri za lugha; lakini kazi hizi zote huzitenda Roho huyo mmoja, yeye yule, akimgawia kila mtu peke yake kama apendavyo yeye.”

 

-          Roho Mtakatifu ni njia ya kurahisisha ukomavu wa kiroho – Roho Mtakatifu anahusika katika kuzaliwa kwetu mara ya pili, lakini pia anahusika katika kusaidia ukomavu wetu wa kiroho, endapo Mkristo atakomaa kiroho matendo yote ya mwili yanapukutika na matunda ya kiroho yanaanza kujichomoza katika maisha ya mwamini, Roho Mtakatifu hatoi karama tu bali anatoa na matunda ambayo kimsingi hutuumbia tabia kama ya Kristo

 

Wagalatia 5:22-25 “Lakini tunda la Roho ni upendo, furaha, amani, uvumilivu, utu wema, fadhili, uaminifu, upole, kiasi; juu ya mambo kama hayo hakuna sheria. Na hao walio wa Kristo Yesu wameusulibisha mwili pamoja na mawazo yake mabaya na tamaa zake. Tukiishi kwa Roho, na tuenende kwa Roho.”

 

-          Roho Mtakatifu hutupa hekima ya utawala na maamuzi – Ili dunia iweze kuongozwa vema na maamuzi yaweze kufanyika kwa haki bila upendeleo wala kuumiza watu tunamuhitaji Roho Mtakatifu ambapo yeye hutoa hofu ya Mungu, haki, ufahamu, ushauri, uweza na maarifa yatakayosaidia kuujenga ufalme wa Mungu na kuiongoza dunia katika haki.

 

Isaya 11:1-5 “Basi litatoka chipukizi katika shina la Yese, na tawi litakalotoka katika mizizi yake litazaa matunda. Na roho ya Bwana atakaa juu yake, roho ya hekima na ufahamu, roho ya shauri na uweza, roho ya maarifa na ya kumcha Bwana; na furaha yake itakuwa katika kumcha Bwana; wala hatahukumu kwa kuyafuata ayaonayo kwa macho yake, wala hataonya kwa kuyafuata ayasikiayo kwa masikio yake; bali kwa haki atawahukumu maskini, naye atawaonya wanyenyekevu wa dunia kwa adili; naye ataipiga dunia kwa fimbo ya kinywa chake, na kwa pumzi ya midomo yake atawaua wabaya. Na haki itakuwa mshipi wa viuno vyake, na uaminifu mshipi wa kujifungia.”

 

Matendo 6:3-4 “Basi ndugu, chagueni watu saba miongoni mwenu, walioshuhudiwa kuwa wema, wenye kujawa na Roho, na hekima, ili tuwaweke juu ya jambo hili; na sisi tutadumu katika kuomba na kulihudumia lile Neno.”

 

-          Roho Mtakatifu hutupa nguvu za kukabiliana na uchawi – Katika ulimwengu huu tulio nao ziko nguvu kubwa mbili zinazotawala, nguvu za Mungu na nguvu za Giza, ili mwanadamu wa kawaida aweze kuwa na nguvu za Mungu zinazoweza kukabiliana na nguvu za giza ni lazima abatizwe katika Roho Mtakatifu, nguvu za Mungu kwetu ziko pia kwaajili ya kukabiliaana na nguvu pinzani  mfano

 

Matendo 13:6-12 “Walipokwisha kupita katikati ya kisiwa chote mpaka Pafo, wakaona mtu mmoja, mchawi, nabii wa uongo, Myahudi jina lake Bar-Yesu; mtu huyu alikuwa pamoja na liwali Sergio Paulo, mtu mwenye akili. Yeye liwali akawaita Barnaba na Sauli waje kwake, akataka kulisikia neno la Mungu. Lakini Elima, yule mchawi (maana ndiyo tafsiri ya jina lake), akashindana nao, akitaka kumtia yule liwali moyo wa kuiacha ile imani. Lakini Sauli, ambaye ndiye Paulo, akijaa Roho Mtakatifu, akamkazia macho, akasema, Ewe mwenye kujaa hila na uovu wote, mwana wa Ibilisi, adui wa haki yote, huachi kuzipotoa njia za Bwana zilizonyoka? Basi, angalia, mkono wa Bwana u juu yako, nawe utakuwa kipofu, usilione jua kwa muda. Mara kiwi kikamwangukia na giza, akazunguka-zunguka na kumtafuta mtu wa kumshika mkono na kumwongoza.Ndipo yule liwali, alipoyaona yaliyotendeka, akaamini, akiyastaajabia mafundisho ya Bwana.”

 

2Timotheo 3:8 “Na kama vile Yane na Yambre walivyopingana na Musa, vivyo hivyo na hawa wanapingana na ile kweli; ni watu walioharibika akili zao, wamekataliwa kwa mambo ya imani.”

 

1Wafalme 18 :21-24 “Naye Eliya akawakaribia watu wote, akanena, Mtasita-sita katikati ya mawazo mawili hata lini? Bwana akiwa ndiye Mungu, mfuateni; bali ikiwa Baali ni Mungu, haya! Mfuateni yeye. Wale watu hawakumjibu neno. Ndipo Eliya akawaambia watu, Mimi nimesalia, mimi peke yangu, nabii wa Bwana; lakini manabii wa Baali ni watu mia nne na hamsini. Kwa hiyo na watutolee ng'ombe wawili; wao na wajichagulie ng'ombe mmoja, wamkate-kate na kumweka juu ya kuni, wasitie moto chini; nami nitamtengeza huyo ng'ombe wa pili, na kumweka juu ya kuni, wala sitatia moto chini. Nanyi ombeni kwa jina la mungu wenu, nami nitaomba kwa jina la Bwana; na Mungu yule ajibuye kwa moto, na awe ndiye Mungu. Watu wote wakajibu wakasema, Maneno haya ni mazuri.”                              

 

Ubatizo wa Roho Mtakatifu.

Fahamu ya kuwa anayebatiza kwa Roho Mtakatifu Ni Bwana Yesu mwenyewe, Na ubatizo huu ni mpango wa Mungu, ni ahadi ya Mungu kwa waaminio kwa hiyo kila mmoja anastahili kupokea kwa Imani na kufungua moyo wake kuhakikisha kuwa maisha yake yanajaa na kufunikwa na uwepo wa Mungu Roho Mtakatifu sawa na neno lake lisemavyo:-

 

a.       Mathayo 3:11 “Kweli mimi nawabatiza kwa maji kwa ajili ya toba; bali yeye ajaye nyuma yangu ana nguvu kuliko mimi, wala sistahili hata kuvichukua viatu vyake; yeye atawabatiza kwa Roho Mtakatifu na kwa moto.”

 

b.       Ubatizo huu ni ahadi ya Mungu mwenyewe kwa kila mtu amwaminiye

Yoel 2:28 “Hata itakuwa, baada ya hayo, ya kwamba nitamimina roho yangu juu ya wote wenye mwili; na wana wenu, waume kwa wake, watatabiri, wazee wenu wataota ndoto, na vijana wenu wataona maono;”

               

Luka 24:49 “Na tazama, nawaletea juu yenu ahadi ya Baba yangu; lakini kaeni humu mjini, hata mvikwe uwezo utokao juu.”

 

Matendo 2:38-39 “Petro akawaambia, Tubuni mkabatizwe kila mmoja kwa jina lake Yesu Kristo, mpate ondoleo la dhambi zenu, nanyi mtapokea kipawa cha Roho Mtakatifu. Kwa kuwa ahadi hii ni kwa ajili yenu, na kwa watoto wenu, na kwa watu wote walio mbali, na kwa wote watakaoitwa na Bwana Mungu wetu wamjie.”

 

c.       Lazima uwe na nia ya kutumika – Ubatizo wa Roho Mtakatifu ni kwaajili ya utumishi, Roho wa Mungu anatabia ya kutaharakisha watu kwaajili ya utumishi, Pale tunapokuwa tayari kwa huduma na kukubali kutumika huku na huko Roho Mtakatifu atakuwa radhi nasi, Ubatizo huu hauwafai watu ambao wakataa tu, unawafaa watu ambao wako tayari kwa kazi kwa sababu Roho Hatakupa kutulia

 

Waamuzi 13:24-25 “Basi yule mwanamke akamzaa mtoto mwanamume akamwita jina lake Samsoni, mtoto huyu akakua, Bwana akambarikia. Roho ya Bwana ikaanza kumtaharakisha katika Mahane-dani, katikati ya Sora na Eshtaoli.”

 

Yeremia 47:6-7 “Ee upanga wa Bwana, Siku ngapi zitapita kabla hujatulia? Ujitie katika ala yako; Pumzika, utulie. Utawezaje kutulia, Ikiwa Bwana amekupa agizo? Juu ya Ashkeloni na juu ya pwani, Ndipo alipoyaamuru hayo.”

 

d.       Kwa maombi bila kuchoka – Kama itatokea hujabatizwa katika Roho mtakatifu wakati Fulani huo usiwe mwisho au mwanzo wa kukata tamaa maandiko yanatutia moyo kuendelea kung’ang’ania mpaka tumpokee Roho Mtakatifu, aidha huwezi kupokea Roho Nyingine zaidi ya kile unachokiomba, iko dhana ya watu kufikiri kuwa ukiwekewa mikono wakati wa maombi utapokea roho Nyingine, Mungu atakupoa sawasawa na kuomba kwako

 

Luka 18:9-13 “Nami nawaambia, Ombeni, nanyi mtapewa; tafuteni, nanyi mtaona; bisheni, nanyi mtafunguliwa. Kwa kuwa kila aombaye hupokea; naye atafutaye huona; naye abishaye atafunguliwa. Maana ni yupi kwenu aliye baba, ambaye mwanawe akimwomba mkate, atampa jiwe au samaki, badala ya samaki atampa nyoka? Au akimwomba yai, atampa nge? Basi, ikiwa ninyi mlio waovu mnajua kuwapa watoto wenu vipawa vyema, je! Baba aliye mbinguni hatazidi sana kuwapa Roho Mtakatifu hao wamwombao?

 

e.       Lazima uwe na imani

Maswala yote ya kiroho yanapokelewa kwa Imani, wakati wote mtu akiwa na mashaka hawezi kupokea kitu kutoka kwa Mungu, kwani pasipo Imani haiwezekani kumpendeza Mungu, kwa hiyo Mtu anayemuhitaji Roho wa Mungu ni lazima aombe kwa Imani,

 

Waebrania 11:6 “Lakini pasipo imani haiwezekani kumpendeza; kwa maana mtu amwendeaye Mungu lazima aamini kwamba yeye yuko, na kwamba huwapa thawabu wale wamtafutao.”

 

Wagalatia 3:2 “Nataka kujifunza neno hili moja kwenu. Je! Mlipokea Roho kwa matendo ya sheria, au kwa kusikia kunakotokana na imani?

 

f.         Kuna umuhimu wa kuomba kwa kupaaza sauti – watu wanaoomba kimyakimya maombi ya ubatizo wa Roho Mtakatifu ni vigumu sana kujazwa maandiko yanaonyesha kuwa wale waliobatizwa katika Roho Mtakatifu walikuwa wakiomba kwa sauti ya kusikika kubwa na ndio maana walijazwa na wakasikika wakisema kwa lugha nyingine

Zaburi 81:10 “Mimi ndimi Bwana, Mungu wako, Niliyekupandisha toka nchi ya Misri; Fumbua sana kinywa chako nami nitakijaza.”

 

Matendo 10:45-46 “Na wale waliotahiriwa, walioamini, wakashangaa, watu wote waliokuja pamoja na Petro, kwa sababu Mataifa nao wamemwagiwa kipawa cha Roho Mtakatifu. Kwa maana waliwasikia wakisema kwa lugha, na kumwadhimisha Mungu. Ndipo Petro akajibu,”

 

Kwa hiyo baada ya kujifunza namna hii na kusikia neno la Mungu kuhusu Ubatizo wa Roho Mtakatifu unapaswa kuamini na kuyatendea kazi yale yote ambayo umeyasikia na ninakuhakikishia hutakuwa kama ulivyo.

Yesu alisisitiza juu ya ahadi hii ya ujio wa Roho Mtakatifu kwa sababu

Roho Mtakatifu ni Msaidizi mwingine, Roho Mtakatifu ana uwezo wa kubadilisha maisha, Roho Mtakatifu hutuvika uwezo au Nguvu kutoka juu, Roho Mtakatifu atatuongoza katika kweli yote Roho Mtakatifu humshuhudia Yesu Kristo, Roho Mtakatifu hutoa nyenzo za kutendea kazi, Roho Mtakatifu ni njia ya kurahisisha ukomavu wa kiroho, Roho Mtakatifu hutupa hekima ya utawala na maamuzi, Roho Mtakatifu hutupa nguvu za kukabiliana na uchawi, kuna na mambo mengine mengi sana ambayo kibinadamu hatuwezi kuyatakeleza bila msaada wa Roho Mtakatifu hivyo ubatizo wa Roho Mtakatifu unabaki kuwa nyenzo Muhimu sana kwa kanisa tangu jana leo na hata milele. Uongezewe neema unapochukua majukumu ya kulitendea kazi neno la Mungu kivitendo, wako katika utumishi.

Na Rev. Innocent Samuel Kamote

Mkuu wa wajenzi Mwenye hekima             

Jumapili, 17 Mei 2026

Kujikwaa kwa watesi wetu na adui zetu!


Zaburi 27:1-3. “Bwana ni nuru yangu na wokovu wangu, Nimwogope nani? Bwana ni ngome ya uzima wangu, Nimhofu nani? Watenda mabaya waliponikaribia, Wanile nyama yangu, Watesi wangu na adui zangu, Walijikwaa wakaanguka. Jeshi lijapojipanga kupigana nami, Moyo wangu hautaogopa. Vita vijaponitokea, Hata hapo nitatumaini.”


Utangulizi:

Ni muhimu kufahamu kuwa Neno la Mungu yaani maandiko matakatifu yanakiri kupitia mwandishi wa zaburi hii ya kuwa Bwana akiwa nuru na wokovu wetu, haijalishi kuwa maadui zetu na watesi wetu hata wawe wengi kiasi gani na hata wajipange vipi, watajikwaa na kuanguka, hii maana yake ni kuwa kumtegemea Mungu kunasababisha tuendelee kubaki wenye nguvu hata kama kuna mashambulizi makali ya adui kutoka kila kona, Zaburi hii pia inafunua Nguvu za Mungu ambazo maadui walipaswa kujiuliza kwanza katika mipango yao kuwa Mungu yuko na nani kabla ya kuanza kujipanga dhidi yetu kwa mashambulizi yoyote yale, Hakuna mtu mwenye hati miliki ya Mungu ati!

2Samuel 5:17-18 “Na hao Wafilisti waliposikia kwamba wamemtia Daudi mafuta ili awe mfalme juu ya Israeli, Wafilisti wote wakapanda kumtafuta Daudi; naye Daudi akapata habari, akashuka akaenda ngomeni. Basi Wafilisti walikuwa wamekuja na kujitawanya bondeni mwa Warefai. Basi Daudi akauliza kwa Bwana, akisema, Je! Nipande juu ya Wafilisti? Utawatia mkononi mwangu? Naye Bwana akamwambia Daudi, Panda; kwa kuwa hakika nitawatia Wafilisti mikononi mwako.”

Ni makosa makubwa sana kupigana vita, kupanga maovu, na kumshambulia kumsema vibaya na kumchafua, mtu ambaye hujui kama ana Mungu au hana, katika vita vya kiroho ni lazima ujue kuwa unayepigana naye ni mwenye haki au mwovu, kama unayepigana naye Mungu yuko upande wake utakufa vibaya, utasambaratika, utaporomoka, utafutika  na hautakuwepo tena kwa kosa la kipuuzi kama hilo lisilozingatia kanuni na utendaji wa Mungu! Watakatifu waliotutangulia Hasa Daudi ambaye alikuwa mtaalamu wa vita alijifunza kuwa Bwana akiwa upande wako atakusaidia, na wanaokuchukia watashindwa na kusambaratika vibaya, Historia yao itafifia na watatoweka duniani!

Zaburi 118:6-8 “Bwana yuko upande wangu, sitaogopa; Mwanadamu atanitenda nini? Bwana yuko upande wangu, msaidizi wangu, Kwa hiyo nitawaona wanaonichukia wameshindwa. Ni heri kumkimbilia Bwana Kuliko kuwatumainia wanadamu.”

Leo basi kwa uzito mkubwa tutatafakari pamoja somo hili muhimu lenye kichwa Kujikwaa kwa watesi wangu na adui zangu, ambalo linakazia ushindi wa ajabu unaowapata watu wa Mungu dhidi ya adui zao, na tutajifunza somo hili kwa kuzingatia vipengele vitatu muhimu vifuatavyo:-



·         Maana ya kujikwaa kwa watesi.

·         Siri ya kujikwaa kwa watesi wetu na adui zetu.

·         Kujikwaa kwa watesi wetu na adui zetu!


Maana ya kujikwaa kwa watesi.

Zaburi 27:1-3. “Bwana ni nuru yangu na wokovu wangu, Nimwogope nani? Bwana ni ngome ya uzima wangu, Nimhofu nani? Watenda mabaya waliponikaribia, Wanile nyama yangu, Watesi wangu na adui zangu, Walijikwaa wakaanguka. Jeshi lijapojipanga kupigana nami, Moyo wangu hautaogopa. Vita vijaponitokea, Hata hapo nitatumaini.”

Ni muhimu kufahamu kuwa neno linalotumika katika Lugha ya Kiebrania kuelezea watesi ni “Tzoreri” au “Oyevai” ambalo kwa Kiingereza ni enemies au oppressors, au adversaries, Maadui, watesaji, watu wanaotaka kukusababishia mabaya katika maisha au wanaofurahia wewe upatwe na mabaya au wanaopanga mipango mibaya juu yako na wenye kutaka kuchafua au kuharibu kibali ulichonacho  hawa ndio wanaitwa watesi an maadui watu ambao hawakufurahii na wanakupinga hawataki mafanikio yako au wanaogopa wewe kufanikiwa hawa Bwana ameahidi katika neno lake kuwa wanapodhamiria kukufanyia mambo yao au hata kama watafanya mambo yao hatimae watajikwaa

Kujikwaa hasa ni nini? Neno linalotumika kuelezea kujikwaa katika lugha ya Kiebrania ni “Kāshal” ambalo maana yake ni kudhoofishwa, kupoteza nguvu, kurudishwa nyuma, kushindwa kusimama, kukutana na kizuizi, kukutana na kikwazo, kukosa uwiano, kuzimia chini ya shinikizo, kuanguka kwa namna isiyotegemewa kwa kiingereza “stumble” au “Fall” kwa hiyo mtu awaye yote anayepambana na watu wa Mungu au mtu wa Mungu anaweza akaanguka na asiinuke tena, huku sio tu kujikwaa kimwili, lakini ni kuanguka kwa mfumo mzima wa adui, kusambaratika kwa mipango, na mifumo ya utendaji wa maadui kupitia nguvu na msaada wa Mungu kwa mtumishi wake.

Zaburi 18:36-40 “Umezifanyizia nafasi hatua zangu, Na miguu yangu haikuteleza. Nitawafuatia adui zangu na kuwapata, Wala sitarudi nyuma hata wakomeshwe. Nitawapiga-piga wasiweze kusimama, Wataanguka chini ya miguu yangu. Nawe hunifunga mshipi wa nguvu kwa vita, Hunitiishia chini yangu walioniondokea. Naam, adui zangu umewafanya wanipe visogo, Nao walionichukia nimewakatilia mbali.”

Siri ya kujikwaa kwa watesi wetu na adui zetu

Neno la Mungu linafunua siri kubwa ni kwa nini maadui hawakufanikiwa, kwanza maadui hawa walikuwa na chuki kubwa na ya kiwango cha juu, walikuwa wamekusudia kuharibu kabisa au kufutilia mbali hawa hawakuwa maadui wa kawaida bali watu waliodhamiria mabaya na katika kudhamiria kwao mabaya walikuwa kama watu wanaokaribia kula nyama kwa uchu hii ni lugha ya kuonyesha tamaa mbaya ya kusababisha uharibifu mkubwa kwa mtu au watu wa Mungu. Walikuwa ni watesi waliokusudia mabaya lakini walijikwaa, Mipango yao iliharibika, uharibifufu uliwapata kwa ghafla, hofu iliwaingia, akili zao zilipigwa na wakachanganyikiwa, maamuzi yao yaligeuzwa kuwa makosa, roho zao ziliingia hatiani, dhamiri zao ziliwasuta, ushindi wako mtu wa Mungu utageuka kuwa ushuhuda kwao, Mwandishi anaeleza kuwa yeye Bwana ni Nuru yake na wokovu wake, haogopi

Zaburi 27:1-3 “Bwana ni nuru yangu na wokovu wangu, Nimwogope nani? Bwana ni ngome ya uzima wangu, Nimhofu nani? Watenda mabaya waliponikaribia, Wanile nyama yangu, Watesi wangu na adui zangu, Walijikwaa wakaanguka. Jeshi lijapojipanga kupigana nami, Moyo wangu hautaogopa. Vita vijaponitokea, Hata hapo nitatumaini.”

Mungu anapokuwa upande wako hakuna anayeweza kusimama kinyume na wewe, adui awaye yote anapokukaribia anakutana na nguvu za Mungu zisizokuwa za kawaida na bila kujielewa wanaanza kupoteza mwelekeo, Mungu hakuwahi kuacha watu wake waonewe, kila anayejipanga kupigana na mtu wa Mungu atashughulikiwa mpaka wajue ya kuwa wewe una Mungu, kama walidhani wao ndio wana Mungu basi Mungu ataonyesha ni kina nani aliwachagua kwaajili ya utukufu wake, adui watapata somo kali ambalo watasimuliana kizazi na kizazi wataelewa ya kuwa kushindana na Mungu ni kujitafutia kifo, ni kupoteza umaarufu, ni kuangamia na kupotea, ni kujifuta katika ramani ya dunia

Zaburi 103:14-15 “Hakumwacha mtu awaonee, Hata wafalme aliwakemea kwa ajili yao. Akisema, Msiwaguse masihi wangu, Wala msiwadhuru nabii zangu.”

Isaya 54:14-17 “Utathibitika katika haki; utakuwa mbali na kuonewa, kwa maana hutaogopa; na mbali na hofu, kwa maana haitakukaribia. Tazama, yamkini watakusanyana; lakini si kwa shauri langu. Watu wo wote watakaokusanyana juu yako wataanguka kwa ajili yako.Tazama, nimemwumba mhunzi avukutaye moto wa makaa, akatoa silaha kwa kazi yake; nami nimemwumba mharibu ili aharibu. Kila silaha itakayofanyika juu yako haitafanikiwa na kila ulimi utakaoinuka juu yako katika hukumu utauhukumu kuwa mkosa. Huu ndio urithi wa watumishi wa Bwana, na haki yao inayotoka kwangu mimi, asema Bwana.”

1Samuel 2:9-10 “Yeye atailinda miguu ya watakatifu wake; Bali waovu watanyamazishwa gizani, Maana kwa nguvu hakuna atakayeshinda; Washindanao na Bwana watapondwa kabisa; Toka mbinguni yeye atawapigia radi; Bwana ataihukumu miisho ya dunia; Naye atampa mfalme wake nguvu, Na kuitukuza pembe ya masihi wake.”                           

Kujikwaa kwa watesi wangu na adui zangu!

Maandiko yanatuthibitishia ya kwamba kila mtu anayekukusudia mabaya juu yako au anayekukaribia kwa nia ovu Mungu atampa kupoteza mwelekeo, wanaopanga mabaya dhidi yako watakosea hatua zao, wanaotaka kukuangusha au kukupoteza wao ndio watakaopotea, hii ni sheria ya kiroho kama Mungu yuko upande wako, adui anapokuja na kukushambulia au kukukaribia ataharibiwa na uwepo wa Mungu, hili sio tukio la bahati mbaya ni tukio la uhakika, wewe na mimi tutamshukuru Mungu kwaajili ya matendo yake makuu atakayotutendea na anayoendela kuyafanya akihukumu kwa haki dhidi ya wale wanaotuchukia, na kujipanga kinyume nasi wao na kila anachojivunia itakuwa historia  

Zaburi 9:1-4 “Nitamshukuru Bwana kwa moyo wangu wote; Nitayasimulia matendo yako yote ya ajabu;Nitafurahi na kukushangilia Wewe; Nitaliimbia jina lako, Wewe Uliye juu. Kwa sababu adui zangu hurudi nyuma; Hujikwaa na kuangamia mbele zako. Kwa maana umenifanyia hukumu na haki Umeketi kitini pa enzi ukihukumu kwa haki.”

Rev. Innocent Samuel Kamote

Mkuu wa wajenzi mwenye Hekima


Jumapili, 10 Mei 2026

Mimi sina mtu wa kunitia birikani!


Yohana 5:5-8 “Na hapa palikuwa na mtu, ambaye amekuwa hawezi muda wa miaka thelathini na minane.  Yesu alipomwona huyu amelala, naye akijua ya kuwa amekuwa hali hiyo siku nyingi, alimwambia, Wataka kuwa mzima?  Yule mgonjwa akamjibu, Bwana, mimi sina mtu wa kunitia birikani, maji yanapotibuliwa; ila wakati ninapokuja mimi, mtu mwingine hushuka mbele yangu.  Yesu akamwambia, Simama, jitwike godoro lako, uende.”




Utangulizi:

Ni muhimu kufahamu kuwa wakati mwingine hapa duniani mtu anaweza kukwama katika mambo fulani fulani tu kwasababu ya kukosa mtu wa kukusaidia, inawezekana unahitaji matibabu ya tatizo fulani la kiafya na linahitaji fedha nyingi lakini ukakosa mtu, au unatafuta kazi mahali fulani na umehangaika kwa muda mrefu lakini ukaikosa kwa sababu tu huna mtu, wako watu wengi sana wamekwama katika maisha na huduma na mambo mbalimbali kwa sababu tu hawana mtu, usipokuwa na mtu hapa duniani wa kukusaidia wakati mwingine unaweza kujikuta umekwama tu unaweza hata kupitia katika mateso na kuwekewa zengwe kwa sababu huna mtu anayekufahamu.

Kutoka 2:8-10 “Basi akainuka mfalme mpya kutawala Misri, asiyemjua Yusufu. Akawaambia watu wake, Angalieni, watu wa wana wa Israeli ni wengi tena wana nguvu kuliko sisi. Haya! Na tuwatendee kwa akili, wasije wakaongezeka; tena, ikitokea vita, wao nao wasije wakashikamana na adui zetu na kupigana nasi, na kutoka katika nchi hii.”

Wana wa Israel waliteseka sana kule Misri na kugeuzwa kuwa watumwa kwa mateso mazito kwa sababu hakukuwa na mtu aliyewatambua, au asiyetambua mchango wa Yusufu huko nyuma, unapokosa mtu anayekufahamu, anayekujua anayeweza kuwa msaada katika dunia hii ya sasa unaweza kuteseka sana. Katika maandiko ya msingi tunasoma habari za mtu mmoja ambaye jina lake halikuweza kufahamika mara moja, lakini mtu huyu alikuwa amepooza na alikuwa akitarajia kupokea uponyaji kutoka katika kisima kiitwacho Bethzatha mtu huyu amekuwa katika hali hii ya mateso kwa miaka 38 na kwa sababu ya jambo hili alipoteza kila kitu huenda aliishi kwa msaada wa wasamaria wema waliompa chakula lakini haja ya moyo wake haikuweza kutimizwa kwa sababu ilihitaji mtu, na hakukuwa na mtu wa kumjali kwa sababu watu walikuwa na watu wao, unaweza kuteseka kwa miaka mingi sana kwa sababu tu hauna mtu, kuna watu wengi sana wamekwama kwa sababu hawana mtu, jamii haikuoni, marafiki hawahusiki na wewe ndugu hawahusiki na wewe uko peke yako na hakuna wa kukutoa kwa sababu huna mtu! 
        

·         Katika Birika la Bethzatha

·         Mimi sina mtu wa kunitia birikani!

·         Kukosa mtu sio kikwazo kwa Yesu


Katika Birika la Bethzatha

Yohana 5:2-9 “Na huko Yerusalemu penye mlango wa kondoo pana birika, iitwayo kwa Kiebrania Bethzatha, nayo ina matao matano. Ndani ya hayo jamii kubwa ya wagonjwa walikuwa wamelala, vipofu, viwete, nao waliopooza, [wakingoja maji yachemke. Kwa maana kuna wakati ambapo malaika hushuka, akaingia katika ile birika, akayatibua maji. Basi yeye aliyeingia wa kwanza baada ya maji kutibuliwa, akapona ugonjwa wote uliokuwa umempata.] Na hapa palikuwa na mtu, ambaye amekuwa hawezi muda wa miaka thelathini na minane. Yesu alipomwona huyu amelala, naye akijua ya kuwa amekuwa hali hiyo siku nyingi, alimwambia, Wataka kuwa mzima? Yule mgonjwa akamjibu, Bwana, mimi sina mtu wa kunitia birikani, maji yanapotibuliwa; ila wakati ninapokuja mimi, mtu mwingine hushuka mbele yangu. Yesu akamwambia, Simama, jitwike godoro lako, uende. Mara yule mtu akawa mzima, akajitwika godoro lake, akaenda. Nayo ilikuwa ni sabato siku hiyo.”

Katika kisa hiki tunajifunza habari za mtu mmoja aliyekuwa amepooza na kuteseka katika mateso hayo kwa muda wa miaka 38 huku mtu huyu akihitaji uponyaji kabla ya kukutana na Yesu, Neno la Mungu linatueleza kuwa kutokana na haja ya moyo wake kuhitaji uponyaji alipelekwa mahali sahihi kabisa ambapo angeweza kupata uponyaji wake mahali hapo ni katika Birika la Bethzatha, Kimsingi mahali hapo palikuwa ndio mahali sahihi pa kupokea muujiza wake lakini hata hivyo hali yake ilizidi kuwa mbaya na aliendelea kudhoofika siku hadi siku, kimsingi angefia mahali ambapo alitakiwa kupokea uponyaji wake na kinyume chake zaidi aliendelea kusota hapo bila ya msaada kwa nini?

“Bethzatha” lilikuwa  ni jina la Kiyunani la kisima maalumu cha uponyaji ambacho kwa lugha ya Kiebrania na Kiaramu kiliitwa “Bethesda” kimsingi jina hili ni muunganiko wa maneno mawili ya kiebrania Beth na Chesed au Hesed neno Beth ni nyumba House na neno Chesed/Hesed ni Rehema Mercy kwa hiyo yanapounganishwa pamoja maneno hayo unapata neno Bethesda  ambalo maana yake ni nyumba ya rehema (House of Mercy)  hapa palikuwa ni mahali pa ajabu sana kwani kisima hiki kilikuwa jijini Yerusalem katika mlango uitwao Lango la kondoo, kisima hiki kilikuwa na matawi matano ambapo maji ya mvua yalikingwa na kupelekwa katika visima vikubwa viwili hapo kulikuwa na wakati kila siku Malaika wa Bwana alishuka na kuyatibua yale maji na mtu anayekuwa wa kwanza kuingia kwa kuwahi huyu alipokea uponyaji, kwa sababu hiyo wagonjwa wengi sana hususani vipofu, viwete na waliopooza walikusanyika hapo na palikuwa na mashindano makali ya yule atakayefanikiwa kuingia kwanza maji yanapotibuliwa alipona, jambo hili lilipelekea wengine hasa wale waliokuwa dhaifu kusubiria hapo kwa miaka mingi, na kama ulikuwa na mtu basi mtu huyo angelikusaidia kuingia kisimani kwa haraka kabla yaw engine na ungepokea uponyaji na kuondoka zako, sasa hapa alikuweko mtu ambaye amesota kwa miaka 38 na hana mtu wa kumsaidia, kimsingi tunapona kuwa mtu huyu alikuwa mahali sahihi ambapo angepokea uponyaji na angeweza kuhurumiwa lakini kinyume chake mambo hayakuwa hivyo badala ya kupata uponyaji na rehema aliendelea kuteseka, aliendelea kusubiri mtu, mahali hapa pakawa mahali pa ushindani, wenye nguvu walidumbukiza ndugu zao, wasio na nguvu na dhaifu walisubiri na wengine walisubiri miaka wakakata tamaa, ndipo siku hii Yesu alikuja maalumu kwaajili ya mtu huyu!

Yohana 5:6-7 “Yesu alipomwona huyu amelala, naye akijua ya kuwa amekuwa hali hiyo siku nyingi, alimwambia, Wataka kuwa mzima? Yule mgonjwa akamjibu, Bwana, mimi sina mtu wa kunitia birikani, maji yanapotibuliwa; ila wakati ninapokuja mimi, mtu mwingine hushuka mbele yangu.”

Mimi sina mtu wa kunitia birikani!

Tunaona kuwa changamoto kubwa hapa ilikuwa ni mtu, hiki ni kilio cha watu wengi leo wanatamani kufanya mambo fulani ya muhimu katika maisha yao lakini hawana mtu, unatamani kusoma lakini huna mtu wa kukulipia ada, unatamani kupata kazi, Lakini huna mtu wa kukuunganisha, unatamani kuanza huduma lakini huna mtu wa kukusapoti, unatamani kurekodi studio lakini huna mtu, unahitaji kuchapa vitabu vyako lakini huna mtu, unatamani, kuolewa au kuoa lakini hauna mtu, unatamani kufanya biashara lakini huna mtu, unatamani, kupata kiti cha magurudumu lakini hauna mtu, unatamani kwenda shule ya ufundi lakini hauna mtu, unatamani kupata dawa za gharama fulani lakini huna mtu, unatamani kujiendeleza lakini huna mtu, unatamani kujishughulisha na kilimo lakini huna mtu, unatamani kufungua ofisi yako lakini huna mtu, unatamani kuanza biashara lakini huna mtu wa kukupa mtaji, unatamani kulima lakini huna mtu, unatamani kufuga lakini huna mtu, unahitaji kufungua ofisi ya ujuzi ulionao lakini huna mtu, mtu yule aliyepooza alikuwa hana mtu wa kusimama naye, alikuwa hana mtu wa kumuinua, alikuwa hana mtu wa kumuunganisha na fursa iliyokuwa mbele yake, una elimu sahihi kabisa lakini huna mtu, una ujuzi sahihi kabisa lakini huna mtu, umesomea shughuli hiyo lakini huna mtu kwaajili ya haya mtu huyu alikata tamaa, inasikitisha kuwa mtu huyu hakuwa na watu watu walimsahau, watu walimuacha, watu hawakumtafuta watu hawakujishughulisha naye, birikika lilikuwa sahihi, na maji yalikuwa sahihi lakini tatizo lake ilikuwa mtu! Kumbe duniani unaweza ukapata shida kwa sababu huna mtu, unaweza ukasota kwa sababu huna mtu, unaweza ukapoteza muda kwa sababu huna mtu, Yesu aliitambua hali aliyopitia mtu yule na hivyo alikuja moja kwa moja kwa mtu yule tena akijua hali halisi kwamba mtu huyu amekosa huduma kwa sababu hana mtu tena ameteseka muda mrefu amelala pale amepigwa na baridi na ameng’atwa na mbu, Godoro lale limechakaa, amesubiri muda mrefu, mpaka amesahau kuwa anahitaji uzima yeye anaona sababu zake ni watu, unaweza kupita katika hali ngumu sana duniani na wewe ukadhani ni kwa sababu ya watu, nisingelikuwa hivi kama sio mtu, haya yote yamenipata kwa sababu ya watu, watu, mtu, watu, mtu, watu, mtu, watu, mtu, hiki ndio kilio cha watu wengi sana, niko hivi nilivyo leo kwa sababu watu au kwa sababu ya mtu! Nisingelikuwa hivi leo ila ni kwa sababu ya mtu au watu! 

Yohana 5:6-7 “Yesu alipomwona huyu amelala, naye akijua ya kuwa amekuwa hali hiyo siku nyingi, alimwambia, Wataka kuwa mzima? Yule mgonjwa akamjibu, Bwana, mimi sina mtu wa kunitia birikani, maji yanapotibuliwa; ila wakati ninapokuja mimi, mtu mwingine hushuka mbele yangu.”

Kukosa mtu sio kikwazo kwa Yesu

Ni muhimu kuelewa kuwa Yesu alikuja moja kwa moja kwa mtu yule mwenye uhitaji, hatusomi kokote kuwa alitaarifiwa habari zake lakini tunaona kuwa Yesu alikuwa na uelewa kamili, alijua shida ya mtu yule na kwa sababu hiyo alikuja kumsaidia shida yake ilikuwa uzima alikuwa nahitaji uponyaji lakini yeye alikuwa anaona watu, Yesu alimwambia wataka kuwa mzima? Yesu alijua kuwa mtu huyu amekuweko kwenye nyumba ya rehema na wala hakupata rehema, alikuwa karibu na birika, na maji lakini havikuweza kumsaidia, malaika walitibua maji lakini hawakumsaidia mgonjwa kuingia kwenye maji, Yesu alikuja kufanya uhamisho wa mtu yule kutoka hospitalini kwenda nyumbani na kuendelea na shughuli zake, inawezekana unahitaji mtu leo nakujulisha yuko mtu huyu ni Yesu

Yohana 5:6-9 “Yesu alipomwona huyu amelala, naye akijua ya kuwa amekuwa hali hiyo siku nyingi, alimwambia, Wataka kuwa mzima? Yule mgonjwa akamjibu, Bwana, mimi sina mtu wa kunitia birikani, maji yanapotibuliwa; ila wakati ninapokuja mimi, mtu mwingine hushuka mbele yangu. Yesu akamwambia, Simama, jitwike godoro lako, uende. Mara yule mtu akawa mzima, akajitwika godoro lake, akaenda. Nayo ilikuwa ni sabato siku hiyo.”

Kimsingi Yesu anaonyesha kuwa anauwezo wa kuingilia mfumo na kufanya mambo nje ya mfumo, Mungu hafungwi na njia za wanadamu wala njia ulizozizoea, Mungu anaweza kukufanyia jambo hata bila ya msaada wa kibinadamu, Mungu anaweza kufanya jambo peke yake jambo lolote ambalo wanadamu wameshindwa, Mungu haitaji mzunguko, wala hataki kukuchelewesha, Mungu hutenda mambo kwa wakati, Mungu anaweza kugeuza mambo kwa ghafla, dakika moja ya Yesu ni bora kuliko masaa elfu, ya kusubiria mtu, unapokuwa hauna mtu kwa taarifa yako Yesu ndiye anakuwa mtu yule, yeye anachotaka ni wewe kuamka na kuchukua hatua, kukosa msaada sio sababu za Mungu kushindwa kutimiza kusudi lake, Mungu anaposema wewe chukua hatua  yeye anapoona hakuna mtu huchukua hatua yeye mwenyewe

Isaya 59:16 “Akaona ya kuwa hapana mtu, akastaajabu kwa kuwa hapana mwombezi; basi, mkono wake mwenyewe ndio uliomletea wokovu; na haki yake ndiyo iliyomsaidia.”

Zaburi 46:1-3 “Mungu kwetu sisi ni kimbilio na nguvu, Msaada utakaoonekana tele wakati wa mateso. Kwa hiyo hatutaogopa ijapobadilika nchi, Ijapotetemeka milima moyoni mwa bahari. Maji yake yajapovuma na kuumuka, Ijapopepesuka milima kwa kiburi chake.”

Mungu anaweza kufanya yeye mwenyewe bila msaada wa kibinadamu, Mungu anaweza kufungua njia bila connection za wanadamu, wanadamu wanaweza kukusahau, lakini Mungu hawezi kukusahau wala kukuacha, watu wanaweza kukupita lakini Mwokozi hatokupita kamwe, watu wanaweza wasikuone lakini Mungu anakuona, unaweza kukaza macho yako kwa Mungu huko ndiko unakoweza kutoka msaada acha kuwalaumu wanadamu mwangalie Yesu, mwambie Mungu naomba unisimamie wewe mwenyewe, mwambie Mungu naomba muda wangu usipotezwe na watu hata kama nimechelewa wewe ndiye msaada wangu mwambie Bwana njoo moja kwa moja wewe mwenyewe naomba unikwamue hapa nilipo, kwaajili ya watu Eee bwana unipe neema nisiwaangalia bali nikuone wewe na kila ninachikihitaji ee bwana fupisha michakato hii unifanyie njia  katika jina la Yesu Kristo wa Nazareth aliye hai Aamen!   kumbuka Bwana ni mtu wa vita atakupigania katika vita yako

“Roho wa Bwana twakualika utawale, karibu Roho wa Bwana fanya mapenzi ya Bwana”

Rev. Innocent Samuel Kamote

Mkuu wa wajenzi mwenye Hekima

Jumapili, 3 Mei 2026

Ndoa na iheshimiwe na watu wote!


Waebrania 13:4. “Ndoa na iheshimiwe na watu wote, na malazi yawe safi; kwa maana waasherati na wazinzi Mungu atawahukumia adhabu.”




Utangulizi:

Leo tutachukua muda kujifunza kwa kina na mapana na marefu undani wa mafundisho ya Biblia kuhusiana na swala la kuheshimu ndoa, tukio ambalo nyakati za leo, limekuwa likichukuliwa si kwa uzito ule ambao Mungu mwenyewe anautoa katika ndoa, Ndoa za siku hizi zimepoteza heshima kuanzia kwa wanandoa wenyewe na mpaka katika jamii inayozizunguka ndoa kutokana na maarifa katika eneo hili kuwa finyu, Agizo la kuheshimiwa kwa ndoa ni agizo zito linalopewa kipaumbele na Mungu, Neno Iheshimiwe katika lugha ya kiyunani yaani Kigiriki(Koine Greek) linasomeka kama neno “timios” likimaanisha kuwa ndoa ni ya thamani sana, ndoa ni ya heshima kubwa sana, ndoa haipaswi kutiwa unajisi, ndoa inatakiwa kuchukuliwa kwa uzito na kwa utukufu wa Mungu, ndoa haipaswi kuchukuliwa kwa wepesi, kwa hiyo hii ina naana ya kuwa Ndoa sio swala la kuchukuliwa kawaida, bali ni swala la kiadilifu na ni takatifu kwa sababu ndoa ilianzishwa na Mungu mwenyewe kama yanenavyo maandiko:-

Mwanzo 2:18-24 “BWANA Mungu akasema, Si vema huyo mtu awe peke yake, nitamfanyia msaidizi wa kufanana naye. BWANA Mungu akafanyiza kutoka katika ardhi kila mnyama wa msituni, na kila ndege wa angani, akamletea Adamu ili aone atawaitaje; kila kiumbe hai, jina alilokiita Adamu likawa ndilo jina lake. Adamu akawapa majina yao kila mnyama wa kufugwa, na ndege wa angani, na kila mnyama wa mwituni; lakini hakuonekana wa kumsaidia Adamu aliyefanana naye. BWANA Mungu akamletea Adamu usingizi mzito, naye akalala; kisha akatwaa ubavu wake mmoja, akafunika nyama mahali pake, na ule ubavu alioutwaa katika Adamu BWANA Mungu akaufanya mwanamke, akamleta kwa Adamu. Adamu akasema, Sasa huyu ni mfupa katika mifupa yangu, na nyama katika nyama yangu, basi ataitwa mwanamke, kwa maana ametwaliwa katika mwanamume. Kwa hiyo mwanamume atamwacha baba yake na mama yake naye ataambatana na mkewe, nao watakuwa mwili mmoja.”

Kwa msingi huo swala la kuiheshimu ndoa ni agizo la Mungu kwa watu wote waliomo katika ndoa wenyewe na wale ambao bado hawajaingia katika ndoa, na wanajamii wote wanapaswa kuiheshimu, kuithamini na kuepuka kwa namna yoyote ile kuiharibu na kuipotosha ndoa, Kimsingi Mungu anaonya jamii iache kuichezea ndoa, kuidharau na hata kuiharibu, kwa sababu zozote zile yakiwemo majungu, uchochezi na ushawishi mbaya na usiofaa, au kuitia unajisi. Tutajifunza somo hili Ndoa na iheshimiwe na watu wote kwa kuzingatia vipengele vikuu muhimu vitatu vifatavyo:-


·         Maana ya kuheshimiwa kwa ndoa.

·         Kwa nini kuna ulazima na umuhimu wa kuheshimu ndoa.

·         Ndoa na iheshimiwe na watu wote.


Maana ya kuheshimiwa kwa ndoa.

Ili tuweze kuwa na uelewa wa kutosha kuhusu agizo la kibiblia kuhusiana na andiko Ndoa na iheshimiwe na watu wote na malazi yawe safi ni muhimu kwetu tukaangalia andiko hili kwanza kutoka katika lugha yake ya asili ya Kiyunani yaani Kigiriki kisha tulifanyie uchambuzi yakinifu, ili tupate maana na msisitizo ulio wazi kutoka kwenye maandiko hayo. Andiko hili linaweza kuwa na tafasiri hii katika lugha ya Kiswahili, Kiyunani na Kiingereza maandiko yanasomeka kama ifuatavyo:-

Kiswahili: Waebrania 13:4. “Ndoa na iheshimiwe na watu wote, na malazi yawe safi; kwa maana waasherati na wazinzi Mungu atawahukumia adhabu.”

Kiyunani: (Timios ho gamos en pasin, kai hē koitē amiantos; pornous gar kai monoecious krinei ho Theos)

Kiingereza: (Hebrews 13:4 Marriage should be honoured by all and the marriage bed kept pure, for God will judge the adulterer and all the sexually immoral) NIV.

Neno ho gamous – Neno hilo maana yake ni Ndoa ni Muungano halali unaojumuisha mwanamke na mwanaume unaokubalika na kubarikiwa na Mungu, kwa hiyo Biblia haitambui ndoa za jinsia zinazofanana, kwa hiyo kuheshimu ndoa ni pamoja na kuheshimu jinsia husika, na kuunganisha wana ndoa wenye jinsia zinafananazo au waliobadili jinsia katika maisha yao baada ya kuzaliwa ni kufuru! na ni kuivunjia ndoa heshima yake katika ngazi ya juu sana

Neno hē koitē – Neno hili ambalo maana yake limetajwa kama kitanda cha ndoa au marriage bed Kiyunani linamaanisha tendo la ndoa, yaani tendo halali ambalo limehalalishwa kwa wana ndoa, kwa hiyo usafi unaotajwa hapo sio wa kitanda na Godoro, bali Mwandishi anazungumzia uadilifu wa tendo la ndoa katika agano halali la ndoa, kwa hiyo kuingilia ndoa ya mtu na kuitia unajisi ni kosa kubwa linalomuuzunisha Mungu, na sio hivyo tu kutoka nje ya ndoa nalo ni kosa kubwa kwa Mungu

Mwanzo 39:7-9 “Ikawa baada ya mambo hayo, mke wa bwana wake akamtamani Yusufu, akamwambia, Lala nami. Lakini akakataa, akamwambia mke wa bwana wake, Tazama, bwana wangu hajui kitu kilichowekwa kwangu nyumbani, na vyote alivyo navyo amevitia mkononi mwangu. Hakuna mkuu katika nyumba hii kuliko mimi, wala hakunizuilia kitu cho chote ila wewe, kwa kuwa wewe u mkewe. Nifanyeje ubaya huu mkubwa nikamkose Mungu?

Ayubu 31:9-12 “Kama moyo wangu ulishawishwa kwa mwanamke, Nami nimeotea mlangoni pa jirani yangu; Ndipo hapo mke wangu na asage kwa mwingine, Na wengine na wainame juu yake. Kwani hilo lingekuwa kosa kuu; Naam, lingekuwa ni uovu wa kuadhibiwa na waamuzi; Kwa kuwa ni moto uteketezao hata Uharibifu, Nao ungeyang'oa maongeo yangu yote.”  

Neno amiantos – maana yake isiyo na doa, isiyotiwa unajisi, isiyochafuliwa, au isiyosababisha madhara kwa tafasiri ya moja kwa moja ni safi yaani isiyochafuliwa kwa dhambi kwa msingi huo tafasiri ya moja kwa moja ya mstari huu wa msingi maana yake ni kwamba ndoa haipaswi kuwa iliyochafuliwa amiantos kwa kiingereza  “undefiled”, “pure” or “unpolluted” au “harmless”. Isitiwe unajisi wala wewe usijitie unajisi kwa kuingia katika ndoa ya mtu, yaani unaichafua na wewe unachafuka

Walawi 19:20 “Nawe usimkaribie mwanamke kufunua utupu wake wakati wa kutengwa kwa ajili ya unajisi wake. Usilale na mke wa mwenzio, ukajitia unajisi naye.”

Neno monoeciousmaana yake ni tendo la ndoa linalofanyika nje ya agano la ndoa uzinzi, au kuchanganya mbegu za uzazi baina ya wanandoa, kuingizia mtoto asiye halali, katika ndoa ya mtu mwingine, au kuchanganya viungo vya uzazi vya aina mbili katika kiungo kimoja, kuchangia mke, Katika mimea tendo hili linaitwa “hermaphrodite”,ambalo linatafasiriwa hivi kwa kiingereza Hermaphrodite which means male and female reproductive organs in the same individual msichangine mke au mume,

Neno Porneia – Lina maana tendo la ndoa linalofanyika kabla ya agano la ndoa au kwa kuhusisha tamaa au kumtumia mwenzi wako vibaya uchafu au uasherati.  

“Kwa hiyo Muungano halali wa ndoa uheshimiwe na watu wote na tendo la ndoa kati ya wanandoa lisiwe linalotiwa unajisi kwa sababu wazinzi na waasharati Mungu atawahukumia adhabu”

Kwa msingi huo Mstari huu wa msingi na unaojitegemea unahimiza wana ndoa kujitunza kwa uaminifu katika ndoa, wao wenyewe wakiwa mstari wa mbele kuheshimu makubaliano yote ya ndoa yaani lile agano na kuepuka kwa sababu zozote zile za kuleteana uchafu wa kingono, picha chafu za ngono, tamaa mbaya na udanganyifu, huku wanandoa wakionywa kutokuutumia mwili wa mwenzi wako vibaya au kumtumia vibaya, kuishi kwa kuheshimiana, kutokuzaliana watoto haramu, kusikilizana, kujaliana, kupendana na kuwa na nia moja kiroho, kuepuka kufanya au kusababisha tendo la ndoa lifanyike nje ya mapenzi na makusudi ya Mungu au nje ya agano, huku wana jamii wakiagizwa kuheshimu sana ndoa takatifu, na kutokuiingilia ndoa ya mtu mwingine au kuwa sababu ya ndoa takatifu kuvunjika, kuichukulia ndoa kwa heshima kubwa na kutokuvunja viwango vya uadilifu katika ndoa, kutokuingilia na kuharibu, kuingilia na kuvuruga, kuwachafua wana ndoa na kuwaletea fitina ama sababu zozote zile zitakazopelekea kuachana kwao, hiyana wivu, uchonganishi majungu na maneno ya kuwakatisha tamaa au kuwashauri vibaya.

Kwa nini kuna ulazima na umuhimu wa kuheshimu ndoa.

Ndoa ni lazima iheshimiwe kwa sababu imeanzishwa na Mungu mwenyewe kama agano la kudumu ambalo linatupa picha ya uhusiano wa Kristo na Kanisa, Ndoa ndio msingi wa Familia jamii na taifa lolote lile, Kamwe hakuwezi kuwa na jamii duniani bila kuweko kwa ndoa, Katika ndoa ndiko Mungu anakotarajia watoto wakue katika Imani nidhamu na ustaarabu, huwezi kuwa na jamii bora kama hakuna ndoa zilizo bora, kama jamii haiheshimu ndoa tutajipatia jamii zilizo hovyo sana duniani.

Katika nyakati hizi za sasa kwa mujibu wa tafiti za karibuni imebainika kuwa heshima kwa ndoa imeshuka kwa kiwango kikubwa kwa asilimia sitini na nne 64% kwa tafiti za kati ya mwaka 1970 mpaka 2024 watu wengi sana katika nyakati za leo hawajiheshimu wala hawaheshimu ndoa, kuanzia kwa wananandoa wenyewe na kwa jamii nzima, bila kujali umri, heshima au cheo, hofu kuhusu mke wa mtu au mume wa mtu katika jamii imeshuka na jambo hili liko mpaka katika makanisa ya Mungu, wanandoa wa siku hizi wanagombania kwenye mitandao ya kijamii, wazee wa zamani wakati mwingine waliweza kuhitilafiana na hata kuachana na jamii isijue siku hizi kuachana ni matangazo, ni fahari na imefikia hatua hata sasa zimekuwepo sherehe za kuadhimisha talaka, mlipendana wenyewe huko sirini mkaona wenyewe huko mitandaoni mnaenda kuanikana na kupata maoni ya watu wapuuzi wa dunia hii ili iweje? 

Ni kwa nini Jamii inapaswa kuheshimu ndoa kama agizo la kibiblia linavyosema hapa ziko sababu kadhaa

1.       Ndoa ni mpango wa Mungu -  Wazo la ndoa kamwe sio la kibinadamu, Ni Mungu ndiye aliyeanzisha ndoa na Ndoa inaonekana mwanzo kabisa wa uumbaji wa Mungu,  katika agano la kale huu ulikuwa ni mpango halali na kamili wa Mungu katika kuanzisha jamii yenye uadilifu kuelekea kwake kwa hiyo halikuwa wazo la Mwanadamu

Mathayo 19:4-6 “Akajibu, akawaambia, Hamkusoma ya kwamba yeye aliyewaumba mwanzo, aliwaumba mtu mume na mtu mke, akasema, Kwa sababu hiyo, mtu atamwacha babaye na mamaye, ataambatana na mkewe; na hao wawili watakuwa mwili mmoja? Hata wamekuwa si wawili tena, bali mwili mmoja. Basi aliowaunganisha Mungu, mwanadamu asiwatenganishe.”

Kwa maelezo hayo ya Bwana wetu Yesu Kristo na hitimisho lake Alichokiunganisha Mungu mwanadamu asikitenganishe maana yake Mungu anapowakutanisha watu na wakafanikiwa kuoana hawana sababu wala hakuna sababu zinazokubalika kwa wao kuachana mpaka Mungu mwenyewe atakapoamua kumchukua mmoja nyumbani, maana yake ni kuwa Ndoa imeanzishwa na Mungu na inatoka kwa Mungu  na hakuna mwanadamu aliye na kibali cha kuimaliza au kuiachanisha, hili linatakiwa kufahamika hivyo kwa wanandoa wenyewe na wana jamii, unapoingilia mke wa mtu au mume wa mtu maana yake wewe utakuwa na adhabu kubwa sana kwa Mungu na laana kwa sababu unataka kuwa sababu ya watu kutengana, au unaweza kusababisha watu kuachana,kufarakana, Yesu anatufundisha hapa kuwa hata talaka sio mpango wa Mungu iwe watu hao waliooana wameokoka au hawajaokoka Mungu anatambua muungano huo na ameufanya.

2.       Ndoa ni eneo la kukua kiroho na kiadilifu – Mungu ameikusudia ndoa kutokuwa swala la uhusiano pekee bali eneo la ukuaji wa kiroho na maadil na uvumilivui, Ndoa ni njia ya kukua na kumfikia Mungu kwa hiyo mojawapo ya sehemu ya ukuaji wa kiroho na kimaadili ni pamoja na kujenga uhusiano wa karibu kati ya wanandoa na hivyo kusababisha ukaribu na Mungu, ndoa zenye msingi imara wa kiroho na uadilifu zinatengeneza jamii yenye uadilifu na uhusiano mzuri na Mungu, Adam na Hawa walipokosea katika maswala ya kiroho na uadilifu uzao wote wa mwanamke ulipata changamoto zinazoathiri jamii mpaka leo.

Mwanzo 3:1-6 “Basi nyoka alikuwa mwerevu kuliko wanyama wote wa mwitu aliowafanya BWANA Mungu. Akamwambia mwanamke, Ati! Hivi ndivyo alivyosema Mungu, Msile matunda ya miti yote ya bustani? Mwanamke akamwambia nyoka, Matunda ya miti ya bustanini twaweza kula; lakini matunda ya mti ulio katikati ya bustani Mungu amesema, Msiyale wala msiyaguse, msije mkafa. Nyoka akamwambia mwanamke, Hakika hamtakufa, kwa maana Mungu anajua ya kwamba siku mtakayokula matunda ya mti huo, mtafumbuliwa macho, nanyi mtakuwa kama Mungu, mkijua mema na mabaya. Mwanamke alipoona ya kuwa ule mti wafaa kwa chakula, wapendeza macho, nao ni mti wa kutamanika kwa maarifa, basi alitwaa katika matunda yake akala, akampa na mumewe, naye akala.”

3.       Ndoa imewekwa kwa kusudi la kuzuia zinaa – Mojawapo ya sababu za kibiblia ya kuwapo kwa ndoa ni kwaajili ya kuzuia zinaa, na Paulo mtume analizungungumzia hili kwa uwazi kwamba ndoa imewekwa kwaajili ya kuzuia uzinzi na uchafu kwa sababu hiyo sababu zozote zile zinazopelekea uchafu ufanyike na zinaa ifanyike Mungu atahukumu, na ndio maana wana ndoa wanapaswa kuhakikisha amani inakuwepo, na shetani hapati nafasi ya kuharibu ndoa, katika namna ya kushanganza sana nyakati za leo hata pamoja na maandiko kuonya wanandoa wamekuwa wakikomoana kwa kunyimana na kutokuridhishana na kupelekea shetani kupata nafasi ya kuharibu ndoa hii ni namna nyingine pia ya kutokuheshimu ndoa.

 

1Wakoritho 7:2-5 “Lakini kwa sababu ya zinaa kila mwanamume na awe na mke wake mwenyewe, na kila mwanamke na awe na mume wake mwenyewe. Mume na ampe mkewe haki yake, na vivyo hivyo mke na ampe mumewe haki yake. Mke hana amri juu ya mwili wake, bali mumewe; vivyo hivyo mume hana amri juu ya mwili wake, bali mkewe. Msinyimane isipokuwa mmepatana kwa muda, ili mpate faragha kwa kusali; mkajiane tena, Shetani asije akawajaribu kwa kutokuwa na kiasi kwenu.”

 

4.        Ndoa ndio eneo la kwanza la mahusiano na upendo -   Mungu alikusudia ndoa iwe eneo la kwanza la mahusiano na upendo, Mwanadamu ni kiumbe cha kijamii, moja ya changamoto iliyoonekana kabla ya anguko la mwanadamu ilikuwa sio vema mtu huyu awe peke yake kwa hiyo Mungu alitaka awepo mtu mwenye kumfaa Adamu na kutoa huduma ya ushirika na kuanzisha jamii, Uhusiano huu wa ndoa unaruhusu wanandoa kukua katika uhusiano na upendo na imani kwa pamoja kuingilia ndoa ya watu ni kuharibu mpango huu wa upendo wa Mungu na ustawi wa ndoa hizo na kuleta vurugu katika jamii, ndoa iheshimiwe, kuingilia mahusiano ya wengine ni wizi, unaingia kuiba upendo usiokuwa wako, jenga wako acha kuharibu wa wengine, heshimu wako wacha kuharibu wa watu wengine  

Mwanzo 2:18. “BWANA Mungu akasema, Si vema huyo mtu awe peke yake, nitamfanyia msaidizi wa kufanana naye.”

Waefeso 5:22-33 “Enyi wake, watiini waume zenu kama kumtii Bwana wetu. Kwa maana mume ni kichwa cha mkewe, kama Kristo naye ni kichwa cha Kanisa; naye ni mwokozi wa mwili. Lakini kama vile Kanisa limtiivyo Kristo vivyo hivyo wake nao wawatii waume zao katika kila jambo. Enyi waume, wapendeni wake zenu, kama Kristo naye alivyolipenda Kanisa, akajitoa kwa ajili yake; ili makusudi alitakase na kulisafisha kwa maji katika neno; apate kujiletea Kanisa tukufu, lisilo na ila wala kunyanzi wala lo lote kama hayo; bali liwe takatifu lisilo na mawaa. Vivyo hivyo imewapasa waume nao kuwapenda wake zao kama miili yao wenyewe. Ampendaye mkewe hujipenda mwenyewe. Maana hakuna mtu anayeuchukia mwili wake po pote; bali huulisha na kuutunza, kama Kristo naye anavyolitendea Kanisa. Kwa kuwa tu viungo vya mwili wake. Kwa sababu hiyo mtu atamwacha baba yake na mama yake, ataambatana na mkewe na hao wawili watakuwa mwili mmoja. Siri hiyo ni kubwa; ila mimi nanena habari ya Kristo na Kanisa. Lakini kila mtu ampende mke wake kama nafsi yake mwenyewe; wala mke asikose kumstahi mumewe.”

5.       Ndoa ni agano takatifu – Ndoa sio tu ushirika wa kawaida wa kijamii ni agano, Ni agano takatifu linaloapwa au linalomuhusisha Mungu, likiwa limekusudiwa kuwa agano la kudumu na lisilovunjika, kuharibu ndoa kwa sababu zozote zile ikiwepo swala la zinaa na uasherati au talaka, linamleta Mungu katika kuingilia na kuhukumu kwa sababu ya kupuuziwa kwa agano lake, Agano ambalo Mungu ni shahidi

Malaki 2:13-16 “Tena mnatenda haya nayo; mnaifunikiza madhabahu ya Bwana kwa machozi, kwa kulia na kwa kuugua, hata asiiangalie tena hiyo dhabihu, wala kuitakabali mikononi mwenu na kuiridhia. Lakini ninyi mwasema, Ni kwa sababu gani? Ni kwa sababu Bwana amekuwa shahidi kati ya wewe na mke wa ujana wako, uliyemtenda mambo ya hiana, angawa yeye ni mwenzako, na mke wa agano lako. Hakuna mtu mmoja aliyetenda hivi, ambaye alikuwa na ufahamu kidogo. Au je! Kuna mtu mmoja atafutaye mzao mwenye kumcha Mungu? Kwa hiyo jihadharini roho zenu; mtu awaye yote asimtende mke wa ujana wake mambo ya hiana. Maana mimi nakuchukia kuachana, asema Bwana, Mungu wa Israeli; naye aifunikizaye nguo yake kwa udhalimu namchukia, asema Bwana wa majeshi; basi jihadharini roho zenu, msije mkatenda kwa hiana.”                      

6.       Kwa sababu Mungu atahukumu wasioheshimu ndoa – Neno la Mungu katika msingi wa andiko tunalojifunza katika somo hili limetoa onyo kali kwa kosa lolote lile litakalohusika katika kuharibu ndoa, Mungu anaona na atahukumu kama alivyosema kwa hiyo hata kama jamii itapotoka na ikapuuzia mpango huu wa Mungu, Mungu mwenyewe atahukumu vikali Katika amri zake za uadilifu ziko amri mbili ambazo zimewekwa na Mungu kwa kusudi la kuilinda ndoa ndani ya zile amri kumi za uadilifu. Kutoka 20:14. “Usizini.”

Kutoka 20:17 “Usiitamani nyumba ya jirani yako, usimtamani mke wa jirani yako; wala mtumwa wake, wala mjakazi wake, wala ng'ombe wake, wala punda wake, wala cho chote alicho nacho jirani yako.”

Waebrania 13:4. “Ndoa na iheshimiwe na watu wote, na malazi yawe safi; kwa maana waasherati na wazinzi Mungu atawahukumia adhabu.”

Jamii inapaswa kukumbuka kuwa ndoa ni muungano wa Mke na Mume uliowekwa na Mungu, Ndoa ni mali ya wenye ndoa, watu wanapaswa kuiheshimu na kuiogopa ndoa, miaka ya zamani jamii ilikuwa inaogopa sana kusikia mke wa mtu au mume wa mtu anatoka nje ya ndoa yake, miaka ya siku hizi watu wanajionea fahari kutoka nje ya ndoa, upofu wa kijamii umeingia na hawaoni tena uzito wa dhambi ya zinaa, agano la ndoa halijaliwi, hakuna heshima, kwa ndoa nyakati za leo na labda kanisa pia limeacha wajibu wake wa kufundisha na kuonya, Bwana atupe neema kutubu na kukaa katika mstari ulionyooka ambao umekusudiwa na Mungu kwaajili ya ndoa, vijana kwa wazee katika jamii wafundishwe na kuelekezwa kuwa jambo hili litaumiza wengi na kuondoa Baraka za Mungu katika maisha yao endapo watachukulia ndoa kama jambo jepesi na la kawaida na kuzivunjia ndoa heshima.

Ndoa na iheshimiwe na watu wote.

Waebrania 13:4. “Ndoa na iheshimiwe na watu wote, na malazi yawe safi; kwa maana waasherati na wazinzi Mungu atawahukumia adhabu.”

Maandiko yanapoagiza swala zima la kuiheshimu ndoa, yanaagiza kuwa ndoa na iheshimiwe na watu wote, neno watu wote katika Biblia ya kiyunani linasomeka kama neno “Pántōn”  ikimaanisha kuwa ndoa na iheshimiwe na watu wote bila kumtenga yeyoye, hii maana yake wanaopaswa kuiheshimu ndoa ni wana jamii wote ambao kimsingi tunaweza kuwaelezea katika makundi kama sita hivi, yaani wanandoa wenyewe, wasio na ndoa, wazazi wa wana ndoa, Jamii kwa ujumla yaani majirani marafiki na watu wote katika jamii wakiwemo viongozi wa mila na desturi, Kanisa na viongozi wa kiroho, na mifumo yote ya Serikali na utawala wa nchi, makundi hayo yote yanajumuishwa katika agizo la kuiheshimu ndoa kila kundi kwa jinsi yake na kwa namna yake kama neno la Mungu linavyoagiza.

1.       Wanandoa wenyewe – Katika agizo la kuiheshimu ndoa kundi la kwanza kabisa linalopaswa kuiheshimu Ndoa ni wana ndoa wenyewe, ni lazima kila mwanadamu mwanamke na mwanamume wanaoingia kwenye ndoa wawe na ufahamu wa kutosha na akili ya kutosha na ujuzi wa kutosha na hekima ya kutosha kuelewa kuhusu ndoa, ndoa ni nini na kwa nini wameacha wazazi wao na kuanza jumuia mpya ndani yake kuna wajibu gani na ni namna gani wanapaswa kuiheshimu sana ndoa, Kabla hujataka watu wengine waiheshimu ndoa yako kwanza wewe mwenyewe uliyeko kwenye ndoa ni lazima uwe unaiheshimu na kujiheshimu, ziko kanuni zinazoiongoza ndoa na kama wana ndoa wenyewe watakuwa wapumbavu na kutokuziheshimu na kujiheshimu ndoa hiyo itashambuliwa na shetani na kuwa na wavamizi

a.       Lazima wanandoa watoshelezane – Moja ya jambo kubwa na la muhimu linalowaunganisha wana ndoa ni tendo lenyewe la ndoa, tendo hili likifanyika kwa ubora na kwa utoshelevu linaleta amani na utulivu na kuleta utoshelevu, tafiti ziko wazi kuwa changamoto zote au nyingi zinazopelekea kuwako kwa migogoro ya ndoa zimebainisha kuwa ni tendo la Ndoa lenyewe kutokufanyika kwa utoshelevu au wanandoa kutokutoshelezana, wana ndoa wengi hawatoshelezani katika tendo la ndoa, na wengi hawana muda hata wa kufanya maandalizi na wala hawafurahii jambo hili linapelekea mmomonyoko wa uadilifu na kushuka kwa heshima ya ndoa, wanawake kwa wanaume wanapaswa kuhakikisha kuwa wanatoshelezana.  

Wimbo uliobora 5:15-19 “Unywe maji ya birika lako mwenyewe, Na maji yenye kububujika katika kisima chako. Je! Chemchemi zako zitawanyike mbali, Na mito ya maji katika njia kuu? Yawe yako mwenyewe peke yako, Wala si ya wageni pamoja nawe. Chemchemi yako ibarikiwe; Nawe umfurahie mke wa ujana wako. Ni ayala apendaye na paa apendezaye; Maziwa yake yakutoshe sikuzote; Na kwa upendo wake ushangilie daima.”

b.      Wananandoa hawapaswi kunyimana – Ndoa inapoteza heshima yake sio tu kwa sababu ya kutokutoshelezana lakini pia kwa sababu ya kunyimana, na changamoto hii katika tafiti za ndoa hujitokeza hasa kwa wanawake na baadae wanaume hujibu mapigo kwa kunyimana ni jambo la kusikitisha na kufedhehesha kuwa hata wanawake waliookoka na kupata mafundisho mara kwa mara bado pia huwa wanampa ibilisi nafasi na kuharibu ndoa zao kwa sababu ya tabia endelevu za kunyimana na kutopeana haki ya ndoa bila sababu za msingi, mioyo ya wanaume wengi sana imeumizwa na matukio ya aina hii ambayo kimsingi ni hujuma iliyo wazi kwa ndoa nadhani ni mwanamke mpumbavu tu ndiye anayeweza kumnyima mumewe kinyume na maandiko na kwa kufanya hivyo huyo anakuwa ndio wa kwanza kulivunja agano. Aidha ni marufuku kwa wanandoa kuuziana tendo la ndoa yaani kulitumia tendo hilo kamammadai kuwa usiponifanyia hiki hutapata hii, jambo hili la kuifanyia ndoa biashara ni kosa kama kosa la kunyimana

1Wakorintho 7:3-5 “Mume na ampe mkewe haki yake, na vivyo hivyo mke na ampe mumewe haki yake. Mke hana amri juu ya mwili wake, bali mumewe; vivyo hivyo mume hana amri juu ya mwili wake, bali mkewe. Msinyimane isipokuwa mmepatana kwa muda, ili mpate faragha kwa kusali; mkajiane tena, Shetani asije akawajaribu kwa kutokuwa na kiasi kwenu.”

c.       Wanandoa wenyewe hawapaswi kutendeana mambo ya hiyana – Maandiko yanawaonya wana ndoa kuokutendeana  mambo ya hiyana, kimsingi mambo ya hiyana ni maswala yote ambayo Mungu anachukizwa nayo kwani yanatikisa na kuharibu misingi ya ndoa, na kuharibu uhusiano, kimsingi kama wana ndoa wanaheshimu Ndoa basi hawapaswi kutendeana mambo hayo ambayo nabii Malaki anayatilia mkazo katika agizo la kiungu.

Malaki 2:13-16 “Tena mnatenda haya nayo; mnaifunikiza madhabahu ya Bwana kwa machozi, kwa kulia na kwa kuugua, hata asiiangalie tena hiyo dhabihu, wala kuitakabali mikononi mwenu na kuiridhia. Lakini ninyi mwasema, Ni kwa sababu gani? Ni kwa sababu Bwana amekuwa shahidi kati ya wewe na mke wa ujana wako, uliyemtenda mambo ya hiana, angawa yeye ni mwenzako, na mke wa agano lako. Hakuna mtu mmoja aliyetenda hivi, ambaye alikuwa na ufahamu kidogo. Au je! Kuna mtu mmoja atafutaye mzao mwenye kumcha Mungu? Kwa hiyo jihadharini roho zenu; mtu awaye yote asimtende mke wa ujana wake mambo ya hiana. Maana mimi nakuchukia kuachana, asema Bwana, Mungu wa Israeli; naye aifunikizaye nguo yake kwa udhalimu namchukia, asema Bwana wa majeshi; basi jihadharini roho zenu, msije mkatenda kwa hiana.”

Mambo ya hiyana ambayo tunaweza kuyabainisha ambayo wana ndoa wasioheshimiana huyafanya au huweza kuyafanya na yakazuia maombi yao na ibada zao ni pamoja na kukoseana adabu au heshima, wanandoa wanapaswa kuheshimiana, na kutengeneza mazingira ya kujenga upendo na ushirikiano, lakini wakiwa wanafarakana na kugombana kukoseana heshima jambo hilo linavunja uadilifu wa ndoa na heshima ya ndoa na kuiharibu, sio hivyo tu kila mwanandoa anapaswa kutimiza wajibu wake na majukumu yake, kujali watoto, kujenga familia yenye afya, kujenga Imani thabiti na utii heshima na upendo, wanandoa wanapaswa kuwa mbali kabisa na usaliti, na kuvunja uaminifu, kuwa na mahusiano na wanawake au wanaume wengine kinyume na uadilifu wa ndoa, kupeana talaka, aidha kwa mwanamke kuidai talaka au kwa mwanaume kutoa talaka, Katika nyakati za leo wanawake katika nchi zilizoendelea wameitumia ndoa sio kwa upendo bali kama mtaji ya kwamba akiolewa na mwanaume tajiri ataachana naye baadae ili apate malipo ya kugawana nusu ya mali ya mwanaume ya utajiri wake Mungu alikusudia ndoa ziwe za kudumu na Mungu anachukia kuachana, pia kufunika nguo kwa udhalimu maana yake ni kunyimana tendo la ndoa, au kufanya zinaa na kadhalika haya yote yote pamoja na migogoro, na kukomoana Malaki anayaita mambo ya hiyana kila mmoja katika ndoa ana wajibu wa kuhakikisha kuwa ndoa inaheshimika na inadumu kama Mungu anavyotaka, wote tuna wajibu wa kuzuia mambo yanayoleta migogoro na uharibifu katika ndoa.

d.      Wanandoa wanapaswa kuhakikisha kuwa malazi yanakuwa safi - Neno hē koitē – Neno hili ambalo maana yake limetajwa kama kitanda cha ndoa au marriage bed Kiyunani linamaanisha tendo la ndoa, linapaswa kuwa safi, Usafi unaotajwa hapo ni kutokutiwa unajisi kwa kitanda cha ndoa kwa wana ndoa wenyewe lakini pia inazungumzia usafi wa kawaida na usafi wa tendo lenyewe hii ikiwa na maana ya kuwa lazima tendo la ndoa lifanyike kwa ufasaha, wanandoa wajifunze namna ya kufurahishana kwa kulifanya tendo hili kwa uhodari hii ikiwa ni pamoja na kutumia mitindo tofauti tofauti, “styles” za tendo la ndoa maadamu tu hazihitilafiani na mapenzi ya Mungu, wanandoa wanapaswa kuhakikisha kuwa wanabadilisha mitindo ya kushirikiana tendo hilo, ili kuondoa uchovu na mazoea ya aina moja ya mitindo, wakati mwingine ikibidi hata eneo, wako watu wengine ambao hufikiri kuwa mitindo hii ni dhambi, Lakini Mungu alimuumba mwanadamu na kumpa tendo hili kwa kusudi la kuongezeka na pia kwa kusudi la kufurahia na kuondoa migandamizo ya mawazo ya safari na uchovu wa dunia na kuleta usingizi mzuri Isaka na Rebeka walikuwa na ndoa yenye furaha kwa sababu walikuwa na mitindo tofauti, walikuwa marafiki walikuwa wakicheza pamoja na kutekenyana na kuchezeana michezo ambayo watu walipoona walijua kuwa huyu alikuwa mke na mume  

Mwanzo 26:6-9 “Isaka akakaa katika Gerari. Watu wa mahali hapo wakamwuliza habari za mkewe. Akasema, Ni ndugu yangu huyu maana aliogopa kusema, Ni mke wangu, watu wa nchi wasije wakamwua kwa ajili ya Rebeka; kwa maana alikuwa mzuri wa uso. Ikawa alipokuwa amekaa huko siku nyingi, Abimeleki, mfalme wa Wafilisti, akachungulia dirishani, akamwona Isaka anacheza-cheza na Rebeka mkewe.Abimeleki akamwita Isaka, akasema, Yakini huyu ni mkeo, mbona ulisema, Ni ndugu yangu huyu? Isaka akamwambia, Kwa sababu nalisema, Nisife kwa ajili yake.”

2.       Wasio na Ndoa – Agizo la kuheshimu ndoa pia linawahusu pia wasiokuwa na ndoa hawa nao wameamriwa katika andiko hili la msingi kuithamini na kutokuhusika kuichezea ndoa, Neno la Mungu linawataka wasiooa na wasiolewa kutokutamani mke wa mtu au mume wa mtu, lakini sio hiyo tu wanapaswa kuepuka ngono kabla ya ndoa kwa hiyo hawapaswi kufanya uasherati, tendo la ndoa linapaswa kufanyika ndani ya ndoa halali tu, kulifanya tendo hili kabla ya wakati wake ni dhambi na kunapelekea kutokuwa na heshima katika ndoa, zaidi hawapaswi kuivamia ndoa ya mtu mwingine na hawapaswi kuitumia miili yao kuharibu ndoa, wasiooa au kuolewa wanapaswa kujiepusha na kuufanya uchafu wa aina yoyote ile unaoharibu ndoa hata kama wewe hauko kwenye ndoa waogope wenye ndoa kama tatizo ili usije ukaadhibiwa na Mungu.

Kutoka 20:17 “Usiitamani nyumba ya jirani yako, usimtamani mke wa jirani yako; wala mtumwa wake, wala mjakazi wake, wala ng'ombe wake, wala punda wake, wala cho chote alicho nacho jirani yako.”

Wathesalonike 4:3-4 “Maana haya ndiyo mapenzi ya Mungu, kutakaswa kwenu, mwepukane na uasherati; kila mmoja wenu ajue kuuweza mwili wake katika utakatifu na heshima;”

3.       Wazazi wa wenye ndoa – Mojawapo ya watu wanaoonywa pia na kuagizwa kuiheshimu ndoa ni pamoja na wazazi, wazazi wengi wasio na ufahamu wameharibu sana ndoa za watoto wao kwa sababu ya tabia ya kuingilia uongozi wa wanandoa na kwa sababu hiyo kuchochea migogoro, au wakati mwingine kwa kushindwa kuwasaidia wana ndoa na kutokuwaambia ukweli au kuamua changamoto zao kwa upendeleo, wanandoa wanapoambiwa kuwa mtu atamuacha baba yake na mama yake maana yake, maana yake wao wanapaswa kuanza serikali yao na hivyo wazazi wanapaswa kuwa walezi na washauri wa mbali na sio wenye kuingilia maamuzi  ya wanandoa na kuendelea kuwafanya wachanga siku zote, wazazi wanaosababisha migongano kwa wana ndoa wanavunja moja kwa moja agizo la ndoa na iheshimiwe na watu wote.

Mwanzo 2:23-24 “Adamu akasema, Sasa huyu ni mfupa katika mifupa yangu, na nyama katika nyama yangu, basi ataitwa mwanamke, kwa maana ametwaliwa katika mwanamume. Kwa hiyo mwanamume atamwacha baba yake na mama yake naye ataambatana na mkewe, nao watakuwa mwili mmoja.”

4.       Jamii kwa ujumla, marafiki, majirani, viongozi wa mila na desturi – Maandiko yapoagiza kuwa ndoa na iheshimiwe na watu wote inawataka wana jamii wote kuheshimu ndoa wakiwemo marafiki, majirani, viongozi wa mila na desturi, wote wanapaswa kuiheshimu ndoa, Viongozi wa kimila ni lazima wasimamie haki na kuondoa mila zote potofu zinazoeneza uzinzi na uasherati kupitia tamaduni za aina mbalimbali, wana jamii wanapaswa kuiheshimu ndoa kwa kutokueneza udaku, habari mbaya na fitina au taariza zinazoweza kuihatarisha ndoa, jamii inapaswa kujiepusha na ushauri mbaya kwa wana ndoa, wanajamii waache maneno maneno na kuwaacha wenye ndoa waishi kwa amani, mtu yeyote anayesambaza habari za kuharibu ndoa ya mtu anafanya dhambi na haiweki ndoa katika vipimo vya Mungu, ziko mila ambazo kundi rika la aina fulani lina uwezo wa kutembea na wake wa wenzake wa rika hilo mila hizo zikomeshwe na hazifai kwani ni kinyume na uadilifu wa ndoa uliowekwa na Mungu, mila zinaweza kuwa bora kama tu hazivunji kanuni na utaratibu uliowekwa na Mungu

Mithali 6:16-19 “Kuna vitu sita anavyovichukia Bwana; Naam, viko saba vilivyo chukizo kwake. Macho ya kiburi, ulimi wa uongo, Na mikono imwagayo damu isiyo na hatia; Moyo uwazao mawazo mabaya; Miguu iliyo myepesi kukimbilia maovu; Shahidi wa uongo asemaye uongo; Naye apandaye mbegu za fitina kati ya ndugu.”

Mithali 12:22-23 “Midomo ya uongo ni chukizo kwa Bwana; Bali watendao uaminifu ndio furaha yake. Mwanadamu mwenye busara husitiri maarifa; Bali moyo wa wapumbavu hutangaza upumbavu

5.       Kanisa na viongozi wa kirohoKanisa na viongozi wa kiroho wanapaswa kukazia na kutokuwa lele mama katika kufundisha uadilifu na uaminifu na utakatifu katika ndoa ni lazima kanisa lisimame katika zamu yake na kuhakikisha ya kuwa maagizo ya Mungu yanafanyiwa kazi katika jamii, na kuwasaidia wana ndoa bila kuziingilia na kuziharibu viongozi wa kanisa ni lazima watumie mamlaka yao vizuri na sio kuharibu ndoa za watu kwani ni makosa kiroho.

Mathayo 19:4-6 “Akajibu, akawaambia, Hamkusoma ya kwamba yeye aliyewaumba mwanzo, aliwaumba mtu mume na mtu mke, akasema, Kwa sababu hiyo, mtu atamwacha babaye na mamaye, ataambatana na mkewe; na hao wawili watakuwa mwili mmoja? Hata wamekuwa si wawili tena, bali mwili mmoja. Basi aliowaunganisha Mungu, mwanadamu asiwatenganishe.”

6.       Serikali na watawala watunga sheria za nchi – Serikali inawajibika kuziheshimu ndoa kwa kuweka taratibu nzuri na kutunga sheria zenye kuilinda jamii na kuilinda ndoa, kwa kuzuia vitendo vya kimapenzi vyenye kusababisha uhalifu ndani yake mfano uzinzi, ubakaji, ulawiti na matendo ya nguvu au uingiliaji wa kingono wa watoto wadogo na kuzuia matendo ya ukahaba mitaani, serikali lazima ilinde Ndoa kwa sheria, mamlaka inapaswa kuisimamia mema kwa mujibu wa neno la Mungu

Warumi 13:1-4 “Kila mtu na aitii mamlaka iliyo kuu; kwa maana hakuna mamlaka isiyotoka kwa Mungu; na ile iliyopo umeamriwa na Mungu. Hivyo amwasiye mwenye mamlaka hushindana na agizo la Mungu; nao washindanao watajipatia hukumu. Kwa maana watawalao hawatishi watu kwa sababu ya matendo mema, bali kwa sababu ya matendo mabaya. Basi, wataka usimwogope mwenye mamlaka? Fanya mema, nawe utapata sifa kwake; kwa kuwa yeye ni mtumishi wa Mungu kwako kwa ajili ya mema. Lakini ufanyapo mabaya, ogopa; kwa maana hauchukui upanga bure; kwa kuwa ni mtumishi wa Mungu, amlipizaye kisasi mtenda mabaya kwa ajili ya ghadhabu.”

Hitimisho:

Neno la Mungu linatoa wito wa kuiheshimu ndoa, wito huu nunaihusua jamii nzima kila mtu anapaswa kutambua kuwa ndoa ni Muungano unaotokana na Mungu  na sio wa kibinadamu, kila mtu anapaswa kuishi kwa uaminifu, usafi, na kuepuka dhambi zinazolichafua agano la ndoa, kuhakikisha kuwa unakuwa mfano wa heshima na upendo wa Kristo na kuhakikisa ya kuwa hugusi mali za watu ili kuepusha laana na kifo katika maisha yako, kila mtu anayegusa ndoa za mtu mwingine anajiweka katika hatari ya hukumu ya Mungu na kifo

Mwanzo 20:1-9 “Ibrahimu akaondoka huko kwenda nchi ya kusini, akakaa kati ya Kadeshi na Shuri, naye akatembea katika Gerari. Ibrahimu akamnena Sara mkewe, Huyu ni ndugu yangu. Basi Abimeleki mfalme wa Gerari akapeleka watu akamtwaa Sara. Lakini Mungu akamjia Abimeleki katika ndoto ya usiku, akamwambia, Umekuwa mfu wewe kwa sababu ya mwanamke huyu uliyemtwaa, maana ni mkewe mtu. Basi Abimeleki alikuwa hakumkaribia, akasema, Ee BWANA, Je! Utaua hata taifa lenye haki? Je! Hakuniambia mwenyewe, Huyu ni ndugu yangu? Na mwanamke mwenyewe naye alisema, Huyu ni ndugu yangu. Kwa ukamilifu wa moyo wangu, na kwa kuwa safi mikono yangu, nimefanya hivi. Mungu akamwambia katika ndoto, Nami nimejua ya kwamba kwa ukamilifu wa moyo wako umefanya hivi, ndipo nami nikakuzuia usinitendee dhambi, kwa hiyo sikukuacha umguse. Basi sasa umrudishe mwanamke kwa mtu huyo, maana yeye ni nabii, naye atakuombea, upate kuishi. Bali usipomrudisha, fahamu ya kwamba kwa hakika utakufa wewe na watu wote ulio nao. Abimeleki akaamka asubuhi na mapema, akawaita watumwa wake wote, akawaambia maneno hayo yote masikioni mwao, nao watu hao wakaogopa sana. Kisha Abimeleki akamwita Ibrahimu, akamwambia, Umetutenda nini? Nimekukosa nini, hata ukaleta juu yangu na juu ya ufalme wangu dhambi kuu? Umenitenda matendo yasiyotendeka.”

Wanandoa wanapaswa kujiepusha kwa namna yoyote ile kujitangaza katika mitandao ya kijamii kama wanaachana, kufanya hivyo kunafungua mlango wa mmomonyoko wa uadilifu, kufungua mlango wa maoni maovu kutoka kwa watu wenye nia mbaya, Kumpa ibilisi nafsi na kupanua wigo wa mashambulizi zaidi, ni jambo la kusikitisha sana kuwa watu waliokuwa wanaishi chumba kimoja na wakati mwingine wana watoto unasikia mitandaoni kuwa wameachana wana simu za mkononi lakini wanajibizania mitandaoni, upumbavu  na ushamba wa namna hii unaweza kufanywa na mabaradhuli tu au watu wasiomjua Mungu, kwa ndoa ya kikristo  na hata isiyo ya kikristo ni muhimu kuweka akiba ya maneno kwani wanandoa wanaweza kurudiana baada ya kuhitilafiana sasa ikiwa mliweka ugomvi wenu na mafarakano yenu mtandaoni ikitokea mnarudiana mtatangaza? Mtataka tena maoni ya jamii nzima yaje kwenye stutus zenu hasa kama ninyi ni wakristo basi tuwe na adabu!

Na. Rev. Innocent Samuel Kamote.

Mkuu wa wajenzi mwenye hekima.