Jumapili, 5 Aprili 2026

Kupandishwa toka shimo la uharibifu!


Zaburi 40:1-3 “Nalimngoja Bwana kwa saburi, Akaniinamia akakisikia kilio changu. Akanipandisha toka shimo la uharibifu, Toka udongo wa utelezi; Akaisimamisha miguu yangu mwambani, Akaziimarisha hatua zangu. Akatia wimbo mpya kinywani mwangu, Ndio sifa zake Mungu wetu. Wengi wataona na kuogopa, Nao watamtumaini Bwana




Utangulizi:

Ni muhimu kufahamu kwamba tuwapo duniani ziko nyakati ambazo tunaweza kupita katika mazingira ya hatari sana, mazingira ya kutisha ambayo kimsingi yanaweza kukuweka katika hali ya kukosa msaada wala hata kusikilizwa kwa sauti yako na ukakosa msaada ni nyakati ambazo unaweza kuchagua kifo kuliko uhai, wakati ambao unaweza kuchagua kukata tamaa kuliko kujipa moyo, nyakati ambazo umezama katika giza na huoni hata dalili ya nuru unachokiona mbele yako ni dalili za uharibifu yaani mauti, hali hiyo inaweza kuwa misiba, inaweza kuwa upotevu wa mali, inaweza kuwa kutapeliwa fedha nyingi, inaweza kuwa changamoto za kiafya inaweza kuwa mashambulizi kutoka kwa maadui, watu wanaokuchukia, inaweza kuwa magonjwa makubwa yasiyo na tiba na kadhalika hayo yanapokushambulia katika lugha ya kibiblia linaitwa shimo la uharibifu, katika nyakati hizo hata Mungu huonekana kuwa kimya unaweza ukamuita na ukasubiri na bado akakunyamazia, kipindi hicho huwa ni kipindi kigumu sana kwa mwanadamu na waandishi wa mashairi ya kibiblia wamekiita shimo la uharibifu! Je umewahi kupita au je unapita katika shimo la uharibifu? wako watu walipita

Zaburi 40:1-3 “Nalimngoja Bwana kwa saburi, Akaniinamia akakisikia kilio changu. Akanipandisha toka shimo la uharibifu, Toka udongo wa utelezi; Akaisimamisha miguu yangu mwambani, Akaziimarisha hatua zangu. Akatia wimbo mpya kinywani mwangu, Ndio sifa zake Mungu wetu. Wengi wataona na kuogopa, Nao watamtumaini Bwana

Katika maandiko yetu ya msingi, tunajifunza ushudua wa Daudi mwandishi wa zaburi hii akimshukuru Mungu baada ya kumuokoa na kumtoa katika shimo la uharibifu, lenye matope na uterezi, kuimarisha hatua zake na kutia wimbo mpya kinywani mwake, Pamoja na kuwa zaburi hii ilimuhusu Daudi, inamuhusu vile vile Yesu Kristo ambaye aliteswa akafa na kuzikwa na kufufuka siku ya tatu akitolewa katika shimo la uharibifu (kaburi), sio hivyo tu zaburi hii inamuhakikishia kila mmoja wetu kuwa Mungu atakutoa katika shimo la uharibifu unalolipitia, tutajifunza somo hili Akanipandisha toka shimo la uharibifu!  kwa kuzingatia vipengele vikuu muhimu vitatu vifuatavyo;-


·         Maana ya shimo la uharibifu

·         Kupandishwa toka shimo la uharibifu

·         Mamlaka ya kupandishwa toka shimoni  


Maana ya shimo la uharibifu.

Shimo la uharibifu katika lugha ya Kiebrania linaitwa “Shâ’ôn bôr” kwa kiingereza ni “Horrible pit” au  “Destruction bore”, au “tumult Pit” au “Sheol” kuzimu au kaburi au hatari ya kifo, ambalo maana yake ni shimo lenye kutisha, au shimo la uharibifu, au shimo la mateso, lenye kelele, lenye kuchanganya, Mwandishi anajaribu kusimulia hali ngumu ambayo Mungu anaweza kuiacha mtu wake akaipitia ambayo kimsingi, ni hali ya shinikizo kubwa sana la mateso ambayo kibinadamu ni vigumu kuyaepuka ni shimo ambalo unanasa na huwezi kujiokoa shimo la utelezi, shimo hili ni kama kuingizwa kaburini ukiwa umekufa ambako sio rahisi kutoka kwa nguvu zako na akili zako za kibinadamu mpaka kwa msaada wa Mungu, Ni Mungu peke yake ndiye anayeweza kukutoa huko!

Zaburi 28:1-2 “Ee Bwana, nitakuita Wewe, mwamba wangu, Usiwe kwangu kama kiziwi. Nisije nikafanana nao washukao SHIMONI, Ikiwa umeninyamalia. Uisikie sauti ya dua yangu nikuombapo, Nikipainulia patakatifu pako mikono yangu.”

Zaburi 88:3-6 “Maana nafsi yangu imeshiba taabu, Na uhai wangu umekaribia kuzimu. Nimehesabiwa pamoja nao washukao SHIMONI; Nimekuwa kama mtu asiye na msaada. Miongoni mwao waliokufa nimetupwa, Kama waliouawa walalao makaburini. Hao ambao Wewe huwakumbuki tena, Wametengwa mbali na mkono wako. Mimi umenilaza katika shimo la chini, Katika mahali penye giza vilindini.”

Zaburi 30:1-3 “Ee Bwana, nitakutukuza kwa maana umeniinua, Wala hukuwafurahisha adui zangu juu yangu. Ee Bwana, Mungu wangu, Nalikulilia ukaniponya. Umeniinua nafsi yangu, Ee Bwana, kutoka KUZIMU. Umenihuisha na kunitoa Miongoni mwao washukao SHIMONI.”

Isaya 38:17-18 “Tazama; nalikuwa na uchungu mwingi kwa ajili ya amani yangu; Lakini kwa kunipenda umeniokoa na SHIMO LA UHARIBIFU; Kwa maana umezitupa dhambi zangu zote nyuma yako. Kwa kuwa KUZIMU hakuwezi kukusifu; mauti haiwezi kukuadhimisha; Wale washukao SHIMONI hawawezi kuitarajia kweli yako.”

Unaona neno shimo katika maandiko au shimo la uharibifu linazungumzia hali ya hatari, hali ya mateso makali, kukata tamaa, hali ya kushindwa na kukandamizwa ni shida na taabu ambazo zinaelekea kelele za mauti na wakati huohuo huwezi kujiokoa au kujitoa katika shimo hilo kwa kuwa ni shimo la matope, hali hii inaweza kufanana kabisa na hali ya mateso aliyoyapitia Bwana wetu Yesu Kristo na kufa kwake msalabani ambapo hakupata msaada wowote wakati wa mateso, kwa hiyo wakati mwingine tunapitia hali kama hiyo ambayo kimsingi tunaweza kufikia kukata tamaa, shimo hili linaweza kuwa shimo la madeni, linaweza kuwa shimo la umasikini, linaweza kuwa shimo la magonjwa, linaweza kuwa shimo la msongo wa mawazo, linaweza kuwa shimo la dhambi, linaweza kuwa shimo la mauti, linaweza kuwa shimo la kushindwa kiroho, linaweza kuwa la matatizo

Kupandishwa toka shimo la uharibifu.

Tunapoadhimisha msimu huu wa pasaka na kufufuka kwa Bwana wetu Yesu Kristo kutoka kwa wafu, tunajikumbusha vile vile kazi ya Mungu ya kuwatoa wanadamu kutoka katika mashimo ya uharibifu mashimo ambayo huwezi kujitoa bila nguvu ya ufufuo, kukutoa katika shimo lako, Yesu alipokufa aliwekwa shimoni na adui zake walililinda na kaburi ili kuhakikisha ya kuwa hatoki humo, Yesu aliingia katika shimo la mateso, alikataliwa na watu jamii nzima ilizomewa jamii ikisema asulubiwe asulubiwe, alipigwa mijeledi, na kuwambwa msalabani akiwa uchi na kufa msalabani na kuzikwa mahali pa giza nene, kaburi lake na mateso yake yalikuwa ni alama ya aibu, kifo, na kushindwa katika macho ya wanadamu, wanadamu wakikuchukia ni kawaida yao kukuweka shimoni

-          Walimuweka Yusufu katika shimo la matope Mwanzo 37:18-24 “Wakamwona toka mbali, na kabla hajawakaribia, wakafanya shauri juu yake ili wamwue. Wakasemezana wao kwa wao, Tazama, yule bwana wa ndoto anakuja. Haya, twende, tukamwue na kumtupa katika birika mojawapo, nasi tutasema, Mnyama mkali amemla; kisha tutaona zitakuwaje ndoto zake. Reubeni akasikia akamwokoa katika mikono yao, akasema, Tusimwue. Reubeni akawaambia, Msimwage damu; mtupeni katika birika hii iliyopo nyikani, wala msimguse; ili apate kumwokoa katika mikono yao, akamrudishe kwa baba yake. Ikawa Yusufu alipofika kwa ndugu zake, wakamvua Yusufu kanzu yake, kanzu ile ndefu aliyoivaa, wakamtwaa wakamtupa katika birika; na hiyo birika ilikuwa tupu, hamna maji.”

 

-          Walimuweka Yeremia katika shimo la matope Yeremia 38:6-9 “Basi wakamtwaa Yeremia, wakamtupa katika shimo la Malkiya, mwana wa mfalme, lililo katika uwanda wa walinzi; wakamshusha kwa kamba. Na mle shimoni hamkuwa na maji, ila matope tu; naye Yeremia akazama katika matope hayo. Basi, Ebedmeleki, Mkushi, towashi, aliyekuwa katika nyumba ya mfalme, aliposikia kama wamemtia Yeremia shimoni; na wakati huo mfalme alikuwa amekaa katika lango la Benyamini; Ebedmeleki akatoka nyumbani mwa mfalme, akamwambia mfalme, akisema,Ee bwana wangu, mfalme, watu hawa wametenda mabaya katika mambo yote waliyomtenda Yeremia, nabii, ambaye wamemtupa shimoni; naye hakosi atakufa pale alipo, kwa sababu ya njaa; kwa kuwa hapana mkate kabisa katika mji.”         

 

-          Walimtupa Daniel katika shimo lenye simba wakali Daniel 6:16-17 “Basi mfalme akatoa amri, nao wakamleta Danieli, wakamtupa katika tundu la simba. Mfalme akanena, akamwambia Danieli, Mungu wako unayemtumikia daima, yeye atakuponya. Likaletwa jiwe, likawekwa mdomoni mwa lile tundu; naye mfalme akalitia muhuri kwa muhuri yake mwenyewe, na kwa muhuri ya wakuu wake, lisibadilike neno lo lote katika habari za Danieli.”

 

Wote waliowekwa shimoni hapo juu walichukiwa, walikataliwa walifanyiwa hila na njama ili ikiwezekana waweze kumalizwa na wasitoke lakini Mungu alikuwa pamoja nao, Daudi pia aliishi mashimoni yaani katika mapango  akitafutwa kuuawa, Yesu Kristo aliwekwa kwenye shimo yaani kaburi, na liliwekwa Muhuri kama la Daniel wote walikuwa wanakabiliwa na mauti, walikandamizwa, walionewa, waliteswa Neno la Mungu linaonyesha ya kuwa ni Mungu mwenyewe ndiye aliyewatoa kutoka katika shimo la uharibifu kama mwandishi wa Zaburi anavyosema

Zaburi 40:1-3 “Nalimngoja Bwana kwa saburi, Akaniinamia akakisikia kilio changu. Akanipandisha toka shimo la uharibifu, Toka udongo wa utelezi; Akaisimamisha miguu yangu mwambani, Akaziimarisha hatua zangu. Akatia wimbo mpya kinywani mwangu, Ndio sifa zake Mungu wetu. Wengi wataona na kuogopa, Nao watamtumaini Bwana

Wakati wa shida yako unapopita katika shimo la uharibifu unaweza kuliitia jina la Bwana naye atakuokoa kutoka shimoni uwezo huo na mamlaka hiyo ya kumtoa mtu kutoka shimoni iko mikononi mwa Mungu, Mwandishi wa zaburi alikuwa katika wakati mgumu aliliitia jina la Bwana na Mungu akikuwa kimya kwa Muda lakini baadae alimchungulia na kisha akamtoa akaimarisha hatua zake, akamuweka juu ya mwamba na kisha akatia wimbo mpya, ni maombi yangu pasaka hii iwe ushuhuda  

Ayubu 33:23-24 “Kwamba akiwapo malaika pamoja naye, Mkalimani, mmoja katika elfu, Ili kumwonyesha binadamu hayo yampasayo; Ndipo amwoneapo rehema, na kusema, Mwokoe asishuke SHIMONI; Mimi nimeuona ukombozi.”

Ayubu 33:28-30 “Yeye ameikomboa nafsi yangu isiende SHIMONI, Na uhai wangu utautazama mwanga. Tazama, hayo yote ni Mungu anayeyafanya, Mara mbili, naam, hata mara tatu, kwa mtu, Ili kurudisha roho yake itoke SHIMONI, Ili atiwe mwanga kwa mwanga wa walio hai.

Yona 2:5-6 “Maji yalinizunguka, hata nafsini mwangu; Vilindi vilinizunguka; Mwani ulikizinga kichwa changu; Nalishuka hata pande za chini za milima; Hiyo nchi na mapingo yake yalinifunga hata milele; Lakini umeipandisha nafsi yangu kutoka SHIMONI, Ee Bwana, Mungu wangu,”

Zaburi 103:3-4 “Akusamehe maovu yako yote, Akuponya magonjwa yako yote, Aukomboa uhai wako na KABURI, Akutia taji ya fadhili na rehema,”          

Mamlaka ya kupandishwa toka shimoni 

Zaburi 40:1-3 “Nalimngoja Bwana kwa saburi, Akaniinamia akakisikia kilio changu. Akanipandisha toka shimo la uharibifu, Toka udongo wa utelezi; Akaisimamisha miguu yangu mwambani, Akaziimarisha hatua zangu. Akatia wimbo mpya kinywani mwangu, Ndio sifa zake Mungu wetu. Wengi wataona na kuogopa, Nao watamtumaini Bwana

Mwandishi wa Zaburi hii yaani Daudi anaonyesha ya kuwa hakuna mwingine anayeweza kumtoa mtu katika shimo la uharibifu isipokuwa Bwana mwenyewe kwa hiyo anasema alimgoja Bwana kwa uvumilivu yaani kwa Saburi, ukombozi wetu unaanza pale tunapoliitia jina la Bwana na kuvumilia yeye ndiye mwenye mamlaka ya kukuchomoa kutoka katika shimo lenye matope, lenye utelezi, yeye anayo mamlaka ya kukutoa katika minyororo, na mazingira yoyote magumu na kubadilisha yale yasiyowezekana na yakawezekana, Hakuna shimo lolote ambalo linaweza kuwa refu kuliko mkono wa Mungu, Mungu anapokutoa hukuweka juu ya mwamba na kuimarisha hatua zako na kukupa ushuhuda mpya wimbo mpya na kila mtu atajifunza kutoka kwako na watu watamtumaini na kumtegemea Mungu, shimo lolote la kushindwa, shimo la dhambi, shimo la mauti, shimo la kukata tamaa, shimo mateso, shimo la madeni, shimo la uharibifu, shimo la aibu, na changamoto.

Katika jina la Yesu Kristo, mwenye mamlaka ya mauti na uzima, mwenye ufunguo wa Daudi naamuru kila mmoja aliyewekwa katika shimo la uharibifu shimo hilo likuachie haraka, shimo la mapepo, shimo la uchawi, shimo la madeni, shimo la kukataliwa, shimo la kusalitiwa, shimo la kuonewa, shimo  la mafarakano, shimo la talaka, shimo na uharibifu katika ndoa, shimo la uharibifu katika familia,  shimo la utumwa wadhambi, shimo la magonjwa sugu, shimo la uonevu naamuru katika jina la Yesu Kristo aliyefufuka kutoka kwa wafu, kila shimo lililokumeza likutapike likuachie katika jina la Yesu Kristo wa Nazareth aliye hai, Bwana akuchomoe katika shimo la matope kama Mchungaji anavyomchomoa Kondoo wake katika jina la Yesu Kristo mwana wa Mungu aliye hai Amen!

Na. Rev. Innocent Samuel Kamote

Mkuu wa wajenzi mwenye Hekima 

Ijumaa, 3 Aprili 2026

Hana umbo wala uzuri hata tumtamani!

 


Isaya 53:2-5 “Maana alikua mbele zake kama mche mwororo, Na kama mzizi katika nchi kavu; Yeye hana umbo wala uzuri; Na tumwonapo hana uzuri hata tumtamani. Alidharauliwa na kukataliwa na watu; Mtu wa huzuni nyingi, ajuaye sikitiko; Na kama mtu ambaye watu humficha nyuso zao, Alidharauliwa wala hatukumhesabu kuwa kitu. Hakika ameyachukua masikitiko yetu, Amejitwika huzuni zetu; Lakini tulimdhania ya kuwa amepigwa, Amepigwa na Mungu, na kuteswa. Bali alijeruhiwa kwa makosa yetu, Alichubuliwa kwa maovu yetu; Adhabu ya amani yetu ilikuwa juu yake, Na kwa kupigwa kwake sisi tumepona.”




Utangulizi:

Leo ni siku ya Ijumaa kuu! Wakristo wote Nchini wanaungana na wakristo wote duniani kukumbuka na kuadhimisha kuteswa, kusulubiwa na kufa msalabani kwa Yesu Kristo wa Nazareth kulikotokea huko nje ya Yerusalem Israel miaka zaidi ya 2000 iliyopita, Katika kujikumbusha tukio hilo kama lilivyotabiriwa na Nabii Isaya zaidi ya miaka 700 kabla ya kuzaliwa kwake, Mateso yake haya yalifanyika dhidi yake huku akiwa hakufanya kosa lolote, lakini maandiko yanaeleza kuwa yalimkuta hayo kwaajili ya uponyaji wa wanadamu kwa sababu imeandika kwa kupigwa kwake sisi tumepona

1Petro 2:22-24 “Yeye hakutenda dhambi, wala hila haikuonekana kinywani mwake. Yeye alipotukanwa, hakurudisha matukano; alipoteswa, hakuogofya; bali alijikabidhi kwake yeye ahukumuye kwa haki. Yeye mwenyewe alizichukua dhambi zetu katika mwili wake juu ya mti, tukiwa wafu kwa mambo ya dhambi, tuwe hai kwa mambo ya haki; na kwa kupigwa kwake mliponywa.”

Kwa msingi huo basi leo tutachukua muda kutafakari na kujifunza kwa kina somo hili “HANA UMBO WALA UZURI HATA TUMTAMANI” kwa kuzingatia vipengele vikuu vitatu muhimu vifuatavyo:-


·         Maana ya neno hana umbo wala uzuri hata tumtamani

·         Yeye hana umbo wala uzuri hata tumtamani

·         Faida ya Mateso ya Bwana wetu Yesu Kristo 


Maana ya neno hana umbo wala uzuri hata tumtamani.

Ni muhimu kufahamu kuwa nabii Isaya alitabiri kuhusu mateso ya Yesu Kristo miaka 700 kabla ya Kristo kuzaliwa na hatimaye unabii wake ulikuja kutimizwa, akimuona katika kioo cha kinabii Isaya anasema kuhusu Masihi katika mateso yake “Yeye hana umbo wala uzuri; Na tumwonapo hana uzuri hata tumtamani.” Maneno haya yana maana gani sasa hebu tuyarejee tena.

Isaya 53:2 “Maana alikua mbele zake kama mche mwororo, Na kama mzizi katika nchi kavu; Yeye hana umbo wala uzuri; Na tumwonapo hana uzuri hata tumtamani.”  

Maneno haya hayamaanishi kamwe kuwa Yesu hakuwa mzuri au hakuwa na mvuto wa kimwili hapana Yesu alikuwa mzuri sana na kijana mwenye mvuto wa kupita kawaida, lakini Isaya anamuona katika kipindi cha mateso yake Yesu akiwa ameharibiwa vibaya na kuchakazwa katika sehemu zote muhimu za mwili wa kibinanadamu, Neno la Kiebrania linalotumika kuelezea umbo ni “tô’ar” na uzuri ni “Hâdâr” ambayo kwa kiingereza ni “appearance” na “majesty” maana yake ni kuwa mwili wake uliharibiwa vibaya sana “disfigured” na heshima yake au utukufu wake ulidhalilishwa na kushushwa kupita maelezo “dishonoured”  kwa hiyo Isaya ni kama anaelezea kuwa wakati wa mateso yake Yesu Kristo hakuna mtu angeweza kutamani kumuona, mateso yale yaliharibu kabisa muonekano wake  na yalidhalilisha kabisa utu wake, hakuwa na utukufu wa kifalme, wala huwezi kutamani kumuona  na kwa sababu hiyo alidharauliwa sana, Mateso yake yalikuwa kama njia ya kumvunjia heshima na kumdhalilisha kabisa na kuharibu heshima yake waliomsulubisha sio tu walikuwa na uwepo wa kishetani lakini pia walimuonea wivu kutokana na uzuri aliokuwa nao na wakakusudia kuuharibu kwa hiyo chuki za waliomsulubisha pia na wivu ulihusika katika kuhakikisha kuwa wanamuharibu kabisa sura yake na kumvunjia kabisa Heshima yake anaelezea mwandishi wa historia wa kiyahudi wa Karne ya kwanza Flavours Josephus walitaka kuhakikisha kuwa anakuwa na huzuni na nafasi ya kujisikitikia

Isaya 53:3-4 “Alidharauliwa na kukataliwa na watu; Mtu wa huzuni nyingi, ajuaye sikitiko; Na kama mtu ambaye watu humficha nyuso zao, Alidharauliwa wala hatukumhesabu kuwa kitu. Hakika ameyachukua masikitiko yetu, Amejitwika huzuni zetu; Lakini tulimdhania ya kuwa amepigwa, Amepigwa na Mungu, na kuteswa.”

Yeye hana umbo wala uzuri hata tumtamani!

Kama tulivyoona maana ya kauli ya hana umbo wala uzuri hata tumtamani ambayo ina maanisha ule uzuri aliokuwa nao Yesu Kristo na utukufu wake uliweza kuharibiwa vibaya kiasi ambacho mtu hangeweza kufikiri kuwa huyu ni mtu au ni mwanadamu yaani aliharibiwa katika namna ambayo ni ngumu kujua kuwa huyu ni mtu yaani watesi walihakikisha wanambomoa uso wake na mwili wake na nafsi yake na roho yake maandiko yanaeleza kuwa aliharibiwa katika kiwango ambacho hakuna mwanadamu aliwahi kuharibiwa hivyo

Isaya 52:14 “Kama vile wengi walivyokustaajabia, (uso wake ulikuwa umeharibiwa sana zaidi ya mtu ye yote, na umbo lake zaidi ya wanadamu),

Isaya 53:5 “Bali alijeruhiwa kwa makosa yetu, Alichubuliwa kwa maovu yetu; Adhabu ya amani yetu ilikuwa juu yake, Na kwa kupigwa kwake sisi tumepona.”    

Watesi wa Yesu Kristo walihakikisha kuwa Yesu anateseka kwa namna zote, anateseka kihisia, kimwili, kijamii, kiroho na kisaikolojia, walimuharibu na kuuchakaza mwili wake kwa mateso ambayo Biblia inaeleza hakuna mtu alichakazwa kwa mtindo na mfumo kama aliofanyiwa Yesu, inawezekana filamu ya “Passion of Christ” ikawa imeonyesha kwa kiwango Fulani uhalisia wa mateso yake, maandiko yakisema aliharibiwa ujue aliharibiwa kweli!  

Kihisia – Yesu alikataliwa na watu wake, alisalitiwa na Yuda Iskariote, kisha wanafunzi wake walimkimbia na wakati wa mateso alibaki peke yake, Petro alimkana mara tatu, mateso haya yakiongozwa na uwepo wa kishetani yalikuwa ni kwaajili ya kusababisha manung’uniko katika moyo wa Yesu apate maumivu ya kihisia na kudhalilika

Yohana 1:10-11 “Alikuwako ulimwenguni, hata kwa yeye ulimwengu ulipata kuwako, wala ulimwengu haukumtambua. Alikuja kwake, wala walio wake hawakumpokea

Mathayo 26:14-16 “Wakati huo mmoja wa wale Thenashara, jina lake Yuda Iskariote, aliwaendea wakuu wa makuhani, akasema, Ni nini mtakachonipa, nami nitamsaliti kwenu? Wakampimia vipande thelathini vya fedha. Tokea wakati huo akawa akitafuta nafasi apate kumsaliti.            

Mathayo 26:56 “Lakini haya yote yamekuwa, ili maandiko ya manabii yatimizwe. Ndipo wanafunzi wote wakamwacha, wakakimbia.”

Luka 22:59-61 “Halafu, yapata saa moja, mtu mwingine alikaza kusema, Hakika na huyu alikuwa pamoja naye, kwa kuwa yeye pia ni Mgalilaya. Petro akasema, Ee mtu, sijui usemalo. Na papo hapo alipokuwa katika kusema, jogoo aliwika. Bwana akageuka akamtazama Petro. Petro akalikumbuka lile neno la Bwana jinsi alivyomwambia, Leo kabla hajawika jogoo utanikana mara tatu.”

Kimwili – Maandiko yanaonyesha kuwa mtumishi wa Mungu (Yesu Kristo) angeteswa katika kiwango ambacho asingeliweza kutambulika, askari wa kirumi walikuwa kama wenye mzuka au walipagawa lilipokuja swala la mateso ya Kristo, walimpiga mijeledi mingi katika namna isiyoweza kuhesabika, walimvika taji ya miiba, huku wakimpiga makofi na kumtemea mate, aliwambwa msalabani akisulubiwa mikono na miguu, kimsingi hakuna mateso makali kama kusulubiwa msalabani, lakini kabla ya hilo wanajeshi wa kirumi walishika mijeledi na kumfunga Yesu kwenye kizimba ambapo unavuliwa nguo na kutandikwa mijeledi, Mijeledi ilikuwa ni fimbo yenye nyuzi kumi na mbili na zile nyuzi zilikuwa na vipande vya vyuma na mifupa ya wanyama wagumu, askari wawili wanaume wenye nguvu walitandika kwa kushindana na wengi waliopitia adhabu hii walichanika tumbo na utumbo ulimwagika nje, unabii wa Isaya na ule wa Daudi katika Zaburi unathibitisha hali mbaya ya mateso ya Kristo namna alivyokuwa

Zaburi 22:14-18 “Nimemwagika kama maji, Mifupa yangu yote imeteguka, Moyo wangu umekuwa kama nta, Na kuyeyuka ndani ya mtima wangu. Nguvu zangu zimekauka kama gae, Ulimi wangu waambatana na taya zangu; Unaniweka katika mavumbi ya mauti, Kwa maana mbwa wamenizunguka; Kusanyiko la waovu wamenisonga; Wamenizua mikono na miguu. Naweza kuihesabu mifupa yangu yote; Wao wananitazama na kunikodolea macho. Wanagawanya nguo zangu, Na vazi langu wanalipigia kura.”             

Yohana 19:1-3 “Basi ndipo Pilato alipomtwaa Yesu, akampiga mijeledi. Nao askari wakasokota taji ya miiba, wakamtia kichwani, wakamvika vazi la zambarau. Wakawa wakimwendea, wakisema, Salamu! Mfalme wa Wayahudi! Wakampiga makofi.”

Mathayo 26:67-68 “Ndipo wakamtemea mate ya uso, wakampiga makonde; wengine wakampiga makofi, wakisema, Ewe Kristo, tufumbulie; ni nani aliyekupiga?

Mathayo 27:29-31 “Wakasokota taji ya miiba, wakaiweka juu ya kichwa chake, na mwanzi katika mkono wake wa kuume; wakapiga magoti mbele yake, wakamdhihaki, wakisema, Salamu, Mfalme wa Wayahudi! Kisha wakamtemea mate, wakautwaa ule mwanzi, wakampiga-piga kichwani. Walipokwisha kumdhihaki, wakalivua lile vazi, wakamvika mavazi yake, wakamchukua kumsulibisha.”

Kijamii - Yesu aliteswa kijamii. Alidhihakiwa hadharani dhidi ya watu wale waliokuwa wakimuheshimu, alihesabiwa pamoja na wahalifu yeye akiwekwa kati kati yao, lakini alivuliwa nguo hadharani tukio hili lilikuwa la udhalilishaji na uaibishaji , jamii hiyo hiyo wakati wa hukumu yake walipiga kelele wakisema asulubiwe asulubiwe!

Isaya 53:12 “Kwa hiyo nitamgawia sehemu pamoja na wakuu, Naye atagawanya nyara pamoja nao walio hodari; Kwa sababu alimwaga nafsi yake hata kufa, Akahesabiwa pamoja na hao wakosao. Walakini alichukua dhambi za watu wengi, Na kuwaombea wakosaji.”        

Yohana 19:23 “Nao askari walipomsulibisha Yesu, waliyatwaa mavazi yake, wakafanya mafungu manne, kwa kila askari fungu lake; na kanzu nayo. Basi kanzu ile haikushonwa, ilikuwa imefumwa yote pia tangu juu.”

Kiroho – kwa kuwa alikuwa amezibeba dhambi za ulimwengu mzima, kwa wakati ule Mungu alikuwa amemuacha, kwa hiyo kwa wakati ule ilikuwa ni kama Mungu amemuacha na kumtenga, Mungu hakumwangalia kama mwanae!

Isaya 59:1-2 “Tazama, mkono wa Bwana haukupunguka, hata usiweze kuokoa wala sikio lake si zito, hata lisiweze kusikia; lakini maovu yenu yamewafarikisha ninyi na Mungu wenu, na dhambi zenu zimeuficha uso wake msiuone, hata hataki kusikia.            

Mathayo 27:45-46 “Basi tangu saa sita palikuwa na giza juu ya nchi yote hata saa tisa. Na kama saa tisa, Yesu akapaza sauti yake kwa nguvu akisema, Eloi, Eloi, lama sabakthani? Yaani, Mungu wangu, Mungu wangu, mbona umeniacha?                         

Faida ya Mateso ya Bwana wetu Yesu Kristo.

Tunapoadhimisha mateso ya Bwana wetu Yesu Kristo aliyeyatoa maisha yake kufa msalabani ni muhimu kwetu kufahamu kuwa Yesu alikubali kufa Msalabani na kuharibiwa vibaya katika namna tuliyojifunza kwa sababu ya makosa yetu na maovu yetu na kwaajili ya tukio hili ziko faida nyingi zinazopatikana kwa kufa kwake Msalabani.

Isaya 53:4-5 “Hakika ameyachukua masikitiko yetu, Amejitwika huzuni zetu; Lakini tulimdhania ya kuwa amepigwa, Amepigwa na Mungu, na kuteswa. Bali alijeruhiwa kwa makosa yetu, Alichubuliwa kwa maovu yetu; Adhabu ya amani yetu ilikuwa juu yake, Na kwa kupigwa kwake sisi tumepona.”

Kwa tendo la Yesu Kristo kufa Msalabani, alizibeba dhambi zetu, na kuwapatanisha wanadamu kwa Mungu kwa kuondoa kiambaza kilichokuwepo kati yetu na Mungu na sio hivyo tu bali aliziharibu nguvu za shetani za kupata mashiko ya kutushitaki akituletea uponyaji wa mwili nafsi na roho lakini kuu kuliko yote ni uzima wa milele

-          Tunapata msamaha wa dhambi kwa sababu aliimwaga damu yake pale msalabani na pasipo kumwagika damu hakuna ondoleo la dhambi

 

Waebrania 9:22 “Na katika Torati karibu vitu vyote husafishwa kwa damu, na pasipo kumwaga damu hakuna ondoleo.”

 

-          Tunapata uponyaji wa mwili nasfi na roho kwa sababu mateso yake yalibeba na kusulubisha magonjwa yetu, maumivu yetu na udhaifu wetu

 

1Petro 2:24 “Yeye mwenyewe alizichukua dhambi zetu katika mwili wake juu ya mti, tukiwa wafu kwa mambo ya dhambi, tuwe hai kwa mambo ya haki; na kwa kupigwa kwake mliponywa.”

 

-          Tunapata Amani ya ndani kabisa iliyopotea, Kila mtu aliyempokea Yesu hata pamoja na kupitia changamoto za aina mbalimbali duniani utaweza kugundua kuwa anapewa Amani ya ndani sana ambayo kimsingi gharama zake zililipwa pale msalabani adhabu aliyopewa ilituletea sisi Amani ya kweli ya maisha ya ndani sana na mwanadamu

 

Amani Isaya 53:4-5 “Hakika ameyachukua masikitiko yetu, Amejitwika huzuni zetu; Lakini tulimdhania ya kuwa amepigwa, Amepigwa na Mungu, na kuteswa. Bali alijeruhiwa kwa makosa yetu, Alichubuliwa kwa maovu yetu; Adhabu ya amani yetu ilikuwa juu yake, Na kwa kupigwa kwake sisi tumepona.”

 

-          Tunaupata ushindi dhidi ya shetani na nguvu zake zote za giza, tendo la kufa kwa Yesu Kristio msalabani baada ya kusulubiwa kwake maaana yake alizivua  enzi  na mamlaka yaani nguvu zake na utendaji wake shetani

 

Wakolosai 2:14-15 “akiisha kuifuta ile hati iliyoandikwa ya kutushitaki kwa hukumu zake, iliyokuwa na uadui kwetu; akaiondoa isiwepo tena, akaigongomea msalabani; akiisha kuzivua enzi na mamlaka, na kuzifanya kuwa mkogo kwa ujasiri, akizishangilia katika msalaba huo.”

 

-          Msalaba ni njia ya uzima huu na uzima wa milele, Kifo cha Yesu kimetuletea uzima wa mwili na uzima wa kiroho  kwa hiyo katika yeye tunao uzima wa milele

 

Yohana 10:10-11 “Mwivi haji ila aibe na kuchinja na kuharibu; mimi nalikuja ili wawe na uzima, kisha wawe nao tele. Mimi ndimi mchungaji mwema. Mchungaji mwema huutoa uhai wake kwa ajili ya kondoo.“

 

1Yohana 5:12-13 “Yeye aliye naye Mwana, anao huo uzima; asiye naye Mwana wa Mungu hana huo uzima. Nimewaandikia ninyi mambo hayo, ili mjue ya kuwa mna uzima wa milele, ninyi mnaoliamini Jina la Mwana wa Mungu.

Hitimisho

Wokovu una gharama kubwa sana umegharimu maisha ya mwana wa Mungu, hatuna budi kuujali na kutokuupuuzia ili tuweze kupona, aliharibiwa namna ile ili sisi tutengenezwe na kufaa mbele za Mungu, basi tuukubali wokovu.

Waebrania 2:2-4 “Kwa maana, ikiwa lile neno lililonenwa na malaika lilikuwa imara, na kila kosa na uasi ulipata ujira wa haki, sisi je! Tutapataje kupona, tusipojali wokovu mkuu namna hii? Ambao kwanza ulinenwa na Bwana, kisha ukathibitika kwetu na wale waliosikia; Mungu naye akishuhudu pamoja nao kwa ishara na ajabu na nguvu za namna nyingi, na kwa magawanyo ya Roho Mtakatifu, kama alivyopenda mwenyewe.”

Na. Rev. Innocent Samuel Kamote

Mkuu wa wajenzi mwenye Hekima       

Jumapili, 29 Machi 2026

Mtoto hajafa Amelala tu !


Marko 5:35-40 “Hata alipokuwa katika kunena, wakaja watu kutoka kwa yule mkuu wa sinagogi, wakisema, Binti yako amekwisha kufa; kwani kuzidi kumsumbua mwalimu? Lakini Yesu, alipolisikia lile neno likinenwa, akamwambia mkuu wa sinagogi, Usiogope, amini tu. Wala hakumruhusu mtu afuatane naye, ila Petro, na Yakobo, na Yohana nduguye Yakobo. Wakafika nyumbani kwa yule mkuu wa sinagogi, akaona ghasia, na watu wakilia, wakifanya maombolezo makuu. Alipokwisha kuingia, akawaambia, Mbona mnafanya ghasia na kulia? Kijana hakufa, bali amelala tu. Wakamcheka sana. Naye alipokwisha kuwatoa nje wote, akamtwaa babaye yule kijana na mamaye, na wale walio pamoja naye, akaingia ndani alimokuwamo yule kijana.



Utangulizi:

Kila mwanadamu mwenye akili timamu huwa anakuwa na ndoto na matarajio kadhaa wa kadha katika maisha, wengine huwa na matarajio makubwa wengine ya wastani na wengine ya kawaida tu katika maisha, kwa kawaida matarajio fulani yasipofikiwa au kutimia katika maisha husababisha msongo mkubwa wa mawazo na wakati mwingine kupoteza kabisa matumaini, matarajio hayo wakati mwingine yanaweza kuwa ya wazi na wakati mwingine yanaweza kuwa ya siri lakini kwa vyo vyote vile yasipofikiwa anayeumia zaidi ni yule aliyekuwa na matumaini hayo. Neno la Mungu lasema

Mithali 13:12 “Kilichotarajiwa kikikawia kuja, moyo huugua. Bali haja ya mtu ikipatikana, ni mti wa uzima.”

Hali hii ilimkuta mtu mmoja muhimu sana katika maandiko, huyu anatajwa kama mojawapo ya wakuu wa sinagogi ambaye alimwendea Yesu wakati binti yake mdogo akiwa katika hali ya kufa, ili yamkini ikiwezekana Yesu aweze kumuhudumia na kuokoa uhai wake aendelee na maisha naye

Marko 5:22-24 “Akaja mtu mmoja katika wakuu wa sinagogi, jina lake Yairo; hata alipomwona, akaanguka miguuni pake, akimsihi sana, akisema, Binti yangu mdogo yu katika kufa; nakuomba uje, uweke mkono wako juu yake, apate kupona, na kuishi. Akaenda pamoja naye; mkutano mkuu wakamfuata, wakimsonga-songa.”

Akiwa katika safari ya kuelekea kumhudumia Yesu alisongwa songwa na watu wengi waliokuwa wakihitaji huduma na zaidi sana tukio la mwanamke mmoja aliyekuwa anatokwa na damu kwa muda wa miaka 13 liliingilia kati na kwa sababu hiyo kuchelewesha safari ya Yesu kufika kwa Yairo, Akiwa katika huduma za dharula zilizokuwa zinaingilia kati, katika huduma za Yesu hapa linakuja kundi la watu na kumpasha habari Yairo kwamba asiendelee kumsumbua Mwalimu kwani binti yake amekwisha kufa!  

Marko 5:35 “Hata alipokuwa katika kunena, wakaja watu kutoka kwa yule mkuu wa sinagogi, wakisema, Binti yako amekwisha kufa; kwani kuzidi kumsumbua mwalimu?

Unapopiga picha ya kile kilichokuwa kinaendelea katika moyo wa Yairo utaweza kugundua kuwa kwa vyovyote vile moyo wake uliugua zaidi na nguvu zake zilimuishia na huenda alikata tamaa, hali kama hii huwapata  baadhi yetu pale yale tunayoyatarajia yanapoonekana kutokuwa na uwezo wa kutimia tena, hali ya kupoteza matumaini inatokea, ndoto zinapokufa, mambo yanapoonekana kutokwenda kama vile tulivyotarajia, afya inapokuwa hatarini, kazi inapoonekana kufika mwisho, mkataba unapoonekana kusimama, kazi uliyoitarajia inapoonekana kufikia mwisho, mchongo unaousikilizia unapoota mbawa, uchumba unapovunjika, mtaji unaposambaratika, mkopo unaposhindwa kulipwa, hasara katika biashara, mavuno usiyoyatarajia na kadhalika wakati huu matumaini huonekana kutoweka  na hiyo iko hivyo katika mtazamo wa Binadamu  Yesu anakuambia usilie kuna matumaini


·         Mungu huona tofauti na wanadamu.

·         Kelele za watu hazibadilishi mpango wa Mungu

·         Mtoto hajafa amelala tu    

          

Mungu huona tofauti na wanadamu

Matarajio ya kila mwanadamu anapopitia changamoto mbalimbali ni pamoja na suluhu ya haraka, kukosa faraja kukumbana na mipaka na kutamani kuondoka katika maumivu yanayotusibu, wakati Mungu mtazamo wake ni wa muda mrefu, wa kutukuza kiroho kutukomaza na kutaka tuuone utukufu wake lakini zaidi sana kuimarisha uhusiano wetu na yeye milele, wanadamu tunaona changamoto kama vikwazo njiani  wakati Mungu anaona vikwazo kama njia ya kuonyesha nguvu na utukufu wake, upendo wake na namna anavyotujali  lakini pia kunyamazisha kelele za kipinzani, wakati watu wanaona mauti kama jambo gumu sana na mwisho wa kila kitu, Yesu anaona mauti ni kama usingizi tu

Isaya 55:8-9 “Maana mawazo yangu si mawazo yenu, wala njia zenu si njia zangu; asema Bwana. Kwa maana kama vile mbingu zilivyo juu sana kuliko nchi, kadhalika njia zangu zi juu sana kuliko njia zenu, na mawazo yangu kuliko mawazo yenu.”

Wakati mwanadamu anawaza kuwa amefika mwisho, Mungu ndio kwanza anaanza jambo, wakati wanadamu wanafikiri kuwa haiwezekani, Mungu anaona kivingine wakati mwanadamu anaona mauti na ukavu, Mungu anaona uhai na upako, Mungu hatendi kazi kwa hisia bali kwa imani!

Ezekiel 37:1-3 “Mkono wa Bwana ulikuwa juu yangu, naye akanichukua nje katika roho ya Bwana, akaniweka chini, katikati ya bonde; nalo limejaa mifupa; akanipitisha karibu nayo pande zote; na tazama, palikuwa na mifupa mingi katika ule uwanda! Nayo, tazama, ilikuwa mikavu sana. Akaniambia, Mwanadamu, je! Mifupa hii yaweza kuishi? Nami nikajibu, Ee Bwana MUNGU, wajua wewe.”         

Mungu alipomuonyesha Ezekiel bonde lililokuwa limejaa mifupa ya wafu na iliyokuwa imekauka sana katika maono yale yeye hakujua kuwa uko uwezekano wa mifupa ile kufanywa hai, hivi ndivyo inavyokuwa wakati mwanadamu anapopitia mambo magumu na hivyo ndivyo ilivyokuwa katika moyo wa Yairo wakati akitarajia uponyaji wa binti yake anapokea taarifa kuwa asimsumbue Mwalimu (Rabbi) kwani binti yake amekwisha kufa, matumaini yake na ya wale waliomletea taarifa yalikuwa yametoweka na sasa kilichokuwa kinasubiriwa ni mipango ya mazishi ya binti wa miaka 12 akiwa anawaza hilo hata hivyo Yesu alikuwa anaona mambo kwa njia nyingine tofauti sana na mtazamo wa kawaida, alimtia moyo Yairio aamini tu asiogope na sio hivyo tu hata alipofika naye kwenye nyumba ya msiba na kuwakataza watu waache kelele za maombolezo kwani mtoto amelala tu wao walimcheka na kumdhihaki wakidhani labda huenda Yesu hajui hata maiti au mtu aliyekufa  

Marko 5:35-36. “Hata alipokuwa katika kunena, wakaja watu kutoka kwa yule mkuu wa sinagogi, wakisema, Binti yako amekwisha kufa; kwani kuzidi kumsumbua mwalimu?Lakini Yesu, alipolisikia lile neno likinenwa, akamwambia mkuu wa sinagogi, Usiogope, amini tu.”

Marko 5:38-39. “Wakafika nyumbani kwa yule mkuu wa sinagogi, akaona ghasia, na watu wakilia, wakifanya maombolezo makuu. Alipokwisha kuingia, akawaambia, Mbona mnafanya ghasia na kulia? Kijana hakufa, bali amelala tu.”

Je wewe unaona nini katika ndoto zako, unaona nini kazini kwako, unaona nini katika ndoa yako, uchumba wako, biashara zako, na maisha yako kwa ujumla, wakati unaona kuwa umefikia mwisho Mungu kwake yeye anaona ndio kwanza mwanzo unaanza, wakati wewe unaona giza yeye ndio kwanza kumekucha kile kinachoonekana kama mwisho kwako ni mapumziko ya muda tu, kamwe usikubali taarifa na tafasiri za watu ziwe tafasiri ya Mungu juu ya maisha yako! Mwangalie Yesu tu.

Kelele za watu hazibadilishi mpango wa Mungu

Walipofika nyumbani kwa Yairo kulikuwa na kelele, waombolezaji walikuwa wameshajaa tayari, na walilia kwa sauti kuu ya maombolezo na ngoma za maombolezo zilikuwa tayari zimeshawekwa  wakati wao wakifanya maombolezo kweli kweli Yesu alikuwa anaona wanafanya ghasia, na aliwakemea na kuwataka waache ghasia zao, wakati mwingine unapokuwa katika wakati mgumu watu wanaokuzunguka wanaweza kuongezea balaa katika majanga yaliyokupata kwani hata kama wewe ulikuwa na matumaini wao wanayafifisha zaidi, kila mmoja anajua kuwa mwisho wa maisha ya mwanadamu ni kifo na kila mtu anaelewa kuwa kifo ndio mwisho wa mambo yote na kwa sababu hiyo waliendelea na maombolezo na masikitiko na vilio ambavyo Yesu aliona kuwa wanafanya ghasia na alipowanyamazisha walimcheka sana, watu na mazingira yanayokuzunguka yanaweza kusema kuwa wewe uwezi tena, wanaweza kusema muda wako umeisha, wanaweza kusema hii ndio imetoka, Lakini Yesu ni kama alikuwa anamwambia Yairo usisikilize sauti za makelele na ghasia za watu wewe sikiliza sauti ya Yesu kelele za watu hazibadilishi mpango wa Mungu kamwe

Marko 5:38-43. “Wakafika nyumbani kwa yule mkuu wa sinagogi, akaona ghasia, na watu wakilia, wakifanya maombolezo makuu. Alipokwisha kuingia, akawaambia, Mbona mnafanya ghasia na kulia? Kijana hakufa, bali amelala tu. Wakamcheka sana. Naye alipokwisha kuwatoa nje wote, akamtwaa babaye yule kijana na mamaye, na wale walio pamoja naye, akaingia ndani alimokuwamo yule kijana. Akamshika mkono kijana, akamwambia, Talitha, kumi; tafsiri yake, Msichana, nakuambia, Inuka. Mara akasimama yule kijana, akaenda; maana alikuwa amepata umri wa miaka kumi na miwili. Mara wakashangaa mshangao mkuu. Akawaonya sana, mtu asijue habari ile; akaamuru apewe chakula.:”

Yesu alimshika mkono aliyekufa na akamwambia msichana nakuambia inuka, Yesu alitumia maeneno ya Kiaramu “Talitha kum” akimaanisha msichana amka, Yesu hakupiga makelele wala hakutaka kufanya muujiza huu kama maonyesho, alikuwa kazini kuwasaidia watu wenye uhitaji, alikuwa kazini kuahirisha msiba, alikuja kusaidia watu, yuko tayari kukusaidia na yuko tayari kukushika mkono, haijalishi moyo wako umepata ganzi kwa kiasi gani wala hijalishi umevunjika moyo kwa kiwango gani, haijalishi umefikia mwisho wa nguvu zako  yeye akikushika mkono uhai utakurudia wakati watu wanadhani imekwisha Yesu anasema inuka, hakuna hali yoyote ile isiyoweza kubadilishwa na Mungu, tumaini lako na ndoto zako haziwezi kuzikwa mbele za Yesu Krito wa Nazareth aliye hai, wakati watu wanafikiri kuwa hali yako itadumu Yesu anaiona hali yako ni ya muda tu kwa sababu hiyo usilie, wala suiogope, acha kutazama mazingira, wala hali yako wala kushindwa kwako kwa Yesu hakuna kitu kinakufa yeye anauwezo wa kuamsha na leo ataliamsha kwenye maisha yako kila jambo linaloonekana kuwa limekufa na watu wameanza kuzomea wakifikiri mwishi umefika, kwa Yesu Kesi yako sio mwisho, kwa Yesu amini tu usiogope kelele za watu hazibadilishi mpango wa Mungu

Mtoto hajafa amelala tu

Katika uwepo wa Mungu kifo ni jambo la muda na sio la milele, wala sio mwisho wa mambo, na ndio Maana Kristo katika mtazamo wake huona kifo kama usingizi tu, wakati wanadamu wanaona ndio mwisho wa kila kitu, Yesu anakiona kifo kama suingizi tu, sio tatizo kubwa yeye ndio huo ufufuo!

Yohana 11:11-14 “Aliyasema hayo; kisha, baada ya hayo, akawaambia, Rafiki yetu, Lazaro, amelala; lakini ninakwenda nipate kumwamsha.Basi wale wanafunzi wakamwambia, Bwana, ikiwa amelala, atapona.Lakini Yesu alikuwa amenena habari ya mauti yake; nao walidhania ya kuwa ananena habari ya kulala usingizi. Basi hapo Yesu akawaambia waziwazi, Lazaro amekufa.”

Yesu alikuwa akionyesha mamlaka yake kama mwana wa Mungu kuwa anao uwezo wa kufufua na ana mamlaka dhidi ya kifo, ni yeye ndiye anayeshikilia funguo (Mamlaka) ya kifo na uzima kwa hiyo yeye anauwezo wa kuwaamsha waliokufa kama anavyoamsha mtu usingizini, Mungu anatumia usemi huu kuwatia moyo wanadamu kuwa kile wanachokiona kama uzito kwake yeye ni chepesi kuliko wanavyofikiri, wanadamu wanapopoteza tumaini wakati wote wanapaswa wakumbuke kuwa yuko Mungu ambaye kwake mambo ni mepesi tu na ndio maana Yesu aliamua kuwatuliza waombolezaji  na kuwafukuzilia mbali na kuwaamuru kuacha ghasia, aidha Yesu alikuwa anataka kuficha mamlaka yake isijulikane na watu nguvu za Mungu sio kwaajili ya maonyesho bali ni kwaajili ya kuwasaidia watu wenye uhitaji, Yesu alikuwa amekuja kuahirisha msiba amkuja kuondoa ghasia

Yesu alichelewa wakati akiwa njiani kumhudumia mtoto wa Yairo ili kutoa muda wa kifo cha mtoto na habari za kifo ziweze kumfikia Yairo nan a majirani na ndugu na jamaa  pia waombolezaji wajikusanye na kufika  na kuanza kuomboleza, wataalamu wa kifo wathibitishe kuwa mtoto amekufa, mwili uoshwe na watu wasubiri amri ya mazishi kutoka kwa baba mzazi wa binti Yairo

Mathayo 9:23-26 “Yesu alipofika nyumbani kwa yule jumbe, aliona wapiga filimbi, na makutano wakifanya maombolezo, akawaambia, Ondokeni; kwa maana kijana hakufa, amelala tu. Wakamcheka sana. Lakini makutano walipoondoshwa, aliingia, akamshika mkono; yule kijana akasimama. Zikaenea habari hizi katika nchi ile yote.”

Mungu anapotaka kufanya mambo ya kushangaza huonekana kama amechelewa ili nguvu zake zionekane kwamba muda sio tatizo kwa Mungu, waombolezaji wakuzunguke ili jina la Mungu litukuzwe, wakati mwingine wambeya watapata habari ya yale yaliyokukuta na watasengenya na kusema Mungu atawaacha wazungumze kuwa jamaa amefikia mwisho  mambo yake yameharibika kwisha habaru yake hawezi kuinuka tena na kadhalika, kisha atafanya muujiza  na hapo kila mtu atajua kuwa Mungu ana uwezo anza kuchangamka ndugu yangu kwa sababu mtoto hajafa amelala tu, kinachokutokea ni kwaajili ya utukufu wa Mungu, yanakutokea ili majirani wapate taarifa, ili ndugu na jmaa wajue ili wasengenyaji wasema wakati wanakuza habari zako hapo anatikea mwanaume anaitwa Yesu anatangaza kuwa msifanye ghasia hapa mtoto hajafa amelala tu !

Yesu pia alkuwa akidhihirisha nguvu zake dhidi ya uumbaji kile anachokitamka ndicho kinachokuwa ni vizuri watu wakaamini katika neno la Mungu kuliko kuzitegemea akili zao wenyewe, Neno la Yesu lina nguvu kwa hiyo anapotamka kuwa ndoto zako hazijakufa zimelala tu ataamsha kila kinachoonekana kufa katika maisha yako, kwa uweza wake wa uumbaji, Yesu alimwamsha binti Yairo ataamsha kila kitu chako kinachoonekana kufa katika maisha yako  na watu wanakudhihaki watazuibwa vinywa vyao, anza kuchangamka kwa sababu mtoto hajafa amelala tu, anza kuzungumza lugha ya Bwana Yesu achana na lugha za waombolezaji hizo ni kelele tu mtoto hajafa amelala tu !

 [Korajabasta, para-kashata, roboboboso-kolotam katerrishetapapapa, kastabastariango, korabashandara-kasto, Yesukarabastanda-ding, koroposhotorabalistakarasto, taraka san sando pang-k-satostamanifesto, roborborboroshosta karabasa]

Mtoto hajafa amelala tu, kila kinachoonekana kufa katika maisha yako Katika jina la Yesu Kristo nakutamkia uzima naifukuza roho ya mauti naachilia uzima kila mahali katika mwili wako, katika ndoa yako, katika nyuimba yako,  katika familia yako, katika biashara yako, kazini kwako, katika afya yako nakutangazia uzima katika jina la Yesu Kristo mwana wa Mungu aliye hai amen! Mungu akutunze!

 

Rev. Innocent Samuel Kamote

Mkuu wa wajenzi mwenye hekima  

Jumapili, 22 Machi 2026

Yuaja mkuu wa ulimwengu huu, wala hana kitu kwangu!


Yohana 14:29-30 “Na sasa nimewaambia kabla halijatokea, kusudi litakapotokea mpate kuamini. Mimi sitasema nanyi maneno mengi tena, kwa maana yuaja mkuu wa ulimwengu huu, wala hana kitu kwangu.”



Utangulizi:

Ni muhimu kufahamu kuwa moja ya maswala ya msingi sana yaliyowahi kutamkwa na Yesu Kristo alipokuwa akiwaandaa wanafunzi wake kwaajili ya kusulubiwa kwake ni pamoja na maneno haya “Yuaja mkuu wa ulimwengu huu, wala hana kitu kwangu” maneno haya yalisemwa masaa machache kabla kidogo ya kukamatwa na maadui zake, kimsingi maneno hayo yalikuwa yanamuhusu Shetani na utendaji wake na kuhusika kwake moja kwa moja katika swala zima la kusulubiwa kwa Yesu Kristo, ambapo Yesu alikuwa akiliona tukio hilo hilo kua ni tukio la ushindi  la hiyari na kuwa ingawa shetani atahusika katika kukamatwa na kusulubiwa kwa Yesu Kristo, Yesu Kristo alikuwa na tafasiri nyingine kuwa litakuwa ni tukio la kuokolewa kwa watu wengi Duniani na ushindi wa kiroho.

Yohana 12:31-33 “Sasa hukumu ya ulimwengu huu ipo; sasa mkuu wa ulimwengu huu atatupwa nje. Nami nikiinuliwa juu ya nchi, nitawavuta wote kwangu. Aliyanena hayo akionyesha ni mauti gani atakayokufa.”

Yohana 13:26-27 “Basi Yesu akajibu, Ndiye mtu yule nitakayemtowelea tonge na kumpa. Akatowelea tonge, akalitwaa akampa Yuda, mwana wa Simoni Iskariote. Na baada ya hilo tonge Shetani alimwingia. Basi Yesu akamwambia, Uyatendayo yatende upesi.”

Njama, mipango na usaliti pamoja na swala zima la kukamatwa kwa Yesu na mpango mzima wa kuteswa kwake na kusulubiwa msalabani kwa namna Fulani kulionekana kama kufaulu kwa mbinu za ibilisi kwani kuliratibiwa chini ya uwepo wa shetani, hata hivyo Yesu anatufungua katika kifungu hiki cha msingi kuwa mpango huo hauna madhara kwake na kuwa ni ushindi wa kiroho wa hali ya juu. Ni kwa msingi huo basi leo tutachukua muda kutafakari kwa pamoja somo hili muhimu Yuaja mkuu wa ulimwengu huu, wala hana kitu kwangu!, tutajifunza somo hili kwa kuzingatia vipengele muhimu vitatu vifuatavyo:-

·         Maana ya neno mkuu wa ulimwengu huu.

·         Yuaja mkuu wa ulimwengu huu.

·         Wala hana kitu kwangu.

Maana ya neno mkuu wa ulimwengu huu.

Yohana 14:29-30 “Na sasa nimewaambia kabla halijatokea, kusudi litakapotokea mpate kuamini. Mimi sitasema nanyi maneno mengi tena, kwa maana yuaja mkuu wa ulimwengu huu, wala hana kitu kwangu.”

Yesu Kristo aliyazungumza maneno hayo muda mfupi kidogo kabla ya kukamatwa kwake na kusulubiwa msalabani kwa mateso mabaya sana, maneno yake hayo yanatufunulia siri nzito kuhusu ushindi utakaoambatana na mateso yake, ushindi unaotokana na kuzizidi hila za shetani na njama zake; Maneno anayoyatumia hapo Mkuu wa ulimwengu huu yana maana gani hasa? Kimsingi neno yuaja mkuu wa ulimwengu huu wala hana kitu kwangu yanasomeka hivi katika lugha ya Kiyunani ona  “yáp archon toutou kósmos erchomai, kai echo oύ oudeis en emoi”  na katika kiingereza cha KJV ambayo ni literal translation Bible yaani ni biblia iliyotafasiriwa kwa mtindo wa neno kwa neno andiko hilo linasomeka hivi  “for the Prince of this world cometh, and hath nothing in me”  NIV yenyewe ambayo ni dynamic translation  inasomeka hivi “for the prince of this world is coming, He has no hold on me” kwa hiyo utabaini kuwa neno Mkuu wa ulimwengu huu au Prince of this world katika Kiyunani anaitwa “Archon” ambalo maana yeke hasa kwa Kiingereza ni “a person in authority” au “a magistrate” kimsingi Yesu alikuwa akimtaja shetani hapo ambaye anatajwa kama mwendesha mashitaka na ushawishi katika mfumo wa ulimwengu huu wa uovu “Ksómos”  taratibu zote za uovu za dunia zinaendeshwa na shetani kwa hiyo kutokana na kazi zake hizo anaitwa mtawala wa dunia hii, au mungu wa dunia hii au mkuu wa anga anayetamalaki falme na mamlaka za kiovu duniani.

Waefeso 2:1-3 “Nanyi mlikuwa wafu kwa sababu ya makosa na dhambi zenu; ambazo mliziendea zamani kwa kuifuata kawaida ya ulimwengu huu, na kwa kumfuata mfalme wa uwezo wa anga, roho yule atendaye kazi sasa katika wana wa kuasi; ambao zamani, sisi sote nasi tulienenda kati yao, katika tamaa za miili yetu, tulipoyatimiza mapenzi ya mwili na ya nia, tukawa kwa tabia yetu watoto wa hasira kama na hao wengine.”

Waefeso 6:10-12 “Hatimaye, mzidi kuwa hodari katika Bwana na katika uweza wa nguvu zake. Vaeni silaha zote za Mungu, mpate kuweza kuzipinga hila za Shetani. Kwa maana kushindana kwetu sisi si juu ya damu na nyama; bali ni juu ya falme na mamlaka, juu ya wakuu wa giza hili, juu ya majeshi ya pepo wabaya katika ulimwengu wa roho.”

Ulimwengu wa uovu uko chini ya utawala na ushawishi na uendeshaji wa kishetani, changamoto na mapambano anayokutana nayo mwanadamu yanayopingana na maisha yetu ya kila siku na mafanikio yetu na uonevu ni matokeo ya kimwili ya kushindana kwetu katika ulimwengu wa kiroho wa utendaji wa shetani ambaye pia huitwa Mungu wa dunia hii.

2Wakorintho 4:3-4 “Lakini ikiwa injili yetu imesitirika, imesitirika kwa hao wanaopotea; ambao ndani yao mungu wa dunia hii amepofusha fikira zao wasioamini, isiwazukie nuru ya injili ya utukufu wake Kristo aliye sura yake Mungu.”

Kwa hiyo Yesu anayasema mambo hayo akiwaonyesha wanafunzi wake kuwa saa yake imewadia ya kwenda kupambana na mkuu wa ulimwengu huu, ni wakati wake sasa kwenda kufanya kazi ambayo kwa akili zake mawazo yake na mpango wake ni kuwa anakwenda kummaliza Yesu Kristo lakini Yesu Kristo katika hekima yake na mpango wake anaonyesha kuwa mpango na mkakati mzima wa ibilisi hautakuwa na mashiko kwake! 

Yuaja mkuu wa ulimwengu huu.

Kwa nini Yesu anatumia neno yuaja? Shetani alikuwa wapi na kwanini Yuaja? Neno yuaja katika Biblia ya kiyunani hapo kama tulivyoona linatumika neno “erchomai” ambalo kwa kiingereza ni “to come” au “to go” ambalo hasa linatumika kuelezea ujio halisi katika mwili  “a Physical movement” kama alikuwa akizunguka zunguka huko na kule katika ulimwengu wa roho sasa anakuja akiwa amejikamilisha kwa hiyo anakuja akijitokeza hadharani “to appear in public” “a physical arrival” kwa hiyo Shetani alikuwa amewapagaa rasmi Yuda, Viongozi wa dini, mahakama na askari wanakuja rasmi sasa kuendesha mateso na kufanya kazi ya kuua kupitia kusulubiwa kikatili, ni muhimu kuelewa hapo kuwa shetani anapokuja wazi kama alivyokuja wakati wa kumkamata Yesu maana yake ni wakati anapowavaa watu na watu hao sasa wanakuwa hawana huruma wanaingiwa na roho ya kikatili, roho mbaya inawakalia huruma ya kibinadamu inaondoka sasa wanakukusudia mabaya, kuharibu kusambaratisha na kuua!

1Petro 5:8-9 “Mwe na kiasi na kukesha; kwa kuwa mshitaki wenu Ibilisi, kama simba angurumaye, huzunguka-zunguka, akitafuta mtu ammeze. Nanyi mpingeni huyo, mkiwa thabiti katika imani, mkijua ya kuwa mateso yale yale yanatimizwa kwa ndugu zenu walioko duniani.”

Ayubu 2:7-8 “Basi Shetani akatoka mbele za uso wa Bwana, akampiga Ayubu na majipu mabaya tangu wayo wa mguu hata utosi wa kichwa. Naye akashika kigae cha kujikunia; akaketi majivuni.”

Yohana 10:10-11 “Mwivi haji ila aibe na kuchinja na kuharibu; mimi nalikuja ili wawe na uzima, kisha wawe nao tele.Mimi ndimi mchungaji mwema. Mchungaji mwema huutoa uhai wake kwa ajili ya kondoo.”

Shetani anapokuja wazi wazi madhara yake yanaonekana wazi wazi, uharibifu mkubwa hutokea, wizi wa Afya mali na uvunjifu mkubwa wa maadili, mafarakano, ukatili uliopitiliza, anapokuja huwa anachinja ni tofauti na Yesu anapokuja, wakati Yesu anapokuja anaokoa, anakuja na uzima wa milele, shetani anapokuja anakuja na kufukuzwa kazi, anakuja na talaka, anakuja na uvamizi, anakuja kuleta hali mbaya, analeta usaliti, analeta mafarakano, kutokuelewana, anakuja na majungu, anakuja na matukio ya kuhuzunisha, hasara, na uhaini, mateso, dharau, matukano na kadhalika  hapo unapoona mambo mabaya yanakuandama kila kitu hakiendi ni kama una nuksi, mikosi na balaa ujue amekuja, Shetani anapokuja maana yake anakuja na kufikia kilele  cha utendaji wa kazi yake katika maisha yetu ataharibu kwa kiasi ambacho unaweza kufikiri kuwa Mungu hana huruma, utashuhudia utendaji wake wa kikatili ambao huwezi kulinganisha na siku au wakati mwingine wowote katika maisha.

Wala hana kitu kwangu.

Yohana 14:29-30 “Na sasa nimewaambia kabla halijatokea, kusudi litakapotokea mpate kuamini. Mimi sitasema nanyi maneno mengi tena, kwa maana yuaja mkuu wa ulimwengu huu, wala hana kitu kwangu.”

Haleluya, habari njema ni kuwa Yesu alitoa taarifa hizo Yuaja mkuu wa ulimwengu huu lakini aliwathibitishia wanafunzi wake kuwa vyo vyote iwavyo hata kama anakuja na saa ile anayokuja inaonekana kuwa ni ya kutisha sana huyu jamaa hana kitu kwake!  Neno wala hana kitu kwangu linasomeka katika Kiyunani “kai echo oύ oudeis en emoi”  kwa kiingereza ESV as “No claim on me” NIV “nothing in me” NASB “ No power over me” KJV “and hath nothing in me” maana yake ni nini hasa anachokimaanisha Yesu ni kuwa pamoja na ujio wake huu wenye hatari wa kumsulubisha mwana wa Mungu Shetani hana udhibiti wowote juu ya Yesu, hana uhalali wowote, hana mamlaka yoyote, wala hausiki kwa lolote wala hana sehemu katika mpango wa Mungu wa ukombozi wa mwanadamu kupitia mauti ya Yesu msalabani Yesu haendi msalabani kwa sababu ya dhambi zake au makosa yake  anaenda kwa mpango wa Mungu kwa hiyari yake mwenyewe, kwani uwezo wa kuutoa uhai anao na uwezo wa kuutwaa anao, hakuna wa kumshitaki Yesu Kristo, uwezo huo uko kwenye mamlaka ya kimbinguni, na sio shetani wala serikali wala makuhani

Yohana 10:17-18 “Ndiposa Baba anipenda, kwa sababu nautoa uhai wangu ili niutwae tena. Hakuna mtu aniondoleaye, bali mimi nautoa mwenyewe. Nami ninao uweza wa kuutoa, ninao na uweza wa kuutwaa tena. Agizo hilo nalilipokea kwa Baba yangu.”

Yohana 19:10-11. “Basi Pilato akamwambia, Husemi nami? Hujui ya kuwa mimi nina mamlaka ya kukufungua, nami nina mamlaka ya kukusulibisha? Yesu akamjibu, Wewe hungekuwa na mamlaka yo yote juu yangu, kama usingepewa kutoka juu; kwa hiyo yeye aliyenitia mikononi mwako yuna dhambi iliyo kubwa zaidi.”

Yohana 8:46-47 “Ni nani miongoni mwenu anishuhudiaye ya kuwa nina dhambi? Nami nikisema kweli, mbona ninyi hamnisadiki? Yeye aliye wa Mungu huyasikia maneno ya Mungu; hivyo ninyi hamsikii kwa sababu ninyi si wa Mungu.”

Waebrania 4:14-15 “Basi, iwapo tunaye kuhani mkuu aliyeingia katika mbingu, Yesu, Mwana wa Mungu, na tuyashike sana maungamo yetu.Kwa kuwa hamna kuhani mkuu asiyeweza kuchukuana nasi katika mambo yetu ya udhaifu; bali yeye alijaribiwa sawasawa na sisi katika mambo yote, bila kufanya dhambi.”

Kitendo cha Yesu kusulubiwa na kufa msalabani kwa mateso makali, hakikutokana na uwezo wa shetani bali ulikuwa ni mpango wa Mungu wa ukombozi wa mwanadamu, kimsingi shetani alihusika kwa upumbavu wake akiwatumia viongozi wa dunia hii waliopagawa na fikra zake, Lakini wakati anajihusisha katika mpango huu alijikaanga kabisa

1Wakorintho 2:6-9 “Walakini iko hekima tusemayo kati ya wakamilifu; ila si hekima ya dunia hii, wala ya hao wanaoitawala dunia hii, wanaobatilika; bali twanena hekima ya Mungu katika siri, ile hekima iliyofichwa, ambayo Mungu aliiazimu tangu milele, kwa utukufu wetu; ambayo wenye kuitawala dunia hii hawaijui hata mmoja; maana kama wangaliijua, wasingalimsulibisha Bwana wa utukufu; lakini, kama ilivyoandikwa, Mambo ambayo jicho halikuyaona wala sikio halikuyasikia, (Wala hayakuingia katika moyo wa mwanadamu,) Mambo ambayo Mungu aliwaandalia wampendao.”

Isaya 53:3-5 “Alidharauliwa na kukataliwa na watu; Mtu wa huzuni nyingi, ajuaye sikitiko; Na kama mtu ambaye watu humficha nyuso zao, Alidharauliwa wala hatukumhesabu kuwa kitu. Hakika ameyachukua masikitiko yetu, Amejitwika huzuni zetu; Lakini tulimdhania ya kuwa amepigwa, Amepigwa na Mungu, na kuteswa. Bali alijeruhiwa kwa makosa yetu, Alichubuliwa kwa maovu yetu; Adhabu ya amani yetu ilikuwa juu yake, Na kwa kupigwa kwake sisi tumepona.”

Yesu alitaka tuelewe ya kuwa vita katika ulimwengu wa roho ni halisi, shetani yuko nyuma ya kila linalokupata anatumia usaliti, mateso na chuki lakini hata hivyo hana kitu kwa Yesu Kristo, sio tu kwa Yesu Kristo bali na kwa kila aaminiye kila mtu anayemkubali Yesu Kristo hapa duniani au ulimwenguni anakuwa kama Yesu kwa hiyo kama yeye alivyo ndivyo tulivyo, kwa hiyo kila yajapo mateso na dhiki za aina yoyote tunajua kuwa amekuja mkuu wa ulimwengu huu lakini hana kitu kwangu, zikija dhiki hivyo hivyo yakija magonjwa wewe jua yanakuja tu lakini hayana kitu kwako kwa sababu wewe ni kama alivyokuwa Kristo hapa duniani una Mungu aliye hai ndani yako

1Yohana 4:15-17 “Kila akiriye ya kuwa Yesu ni Mwana wa Mungu, Mungu hukaa ndani yake, naye ndani ya Mungu. Nasi tumelifahamu pendo alilo nalo Mungu kwetu sisi, na kuliamini. Mungu ni upendo, naye akaaye katika pendo, hukaa ndani ya Mungu, na Mungu hukaa ndani yake. Katika hili pendo limekamilishwa kwetu, ili tuwe na ujasiri katika siku ya hukumu; kwa kuwa, kama yeye alivyo, ndivyo tulivyo na sisi ulimwenguni humu.”

1Yohana 4:4 “Ninyi, watoto wadogo, mwatokana na Mungu nanyi mmewashinda, kwa sababu yeye aliye ndani yenu ni mkuu kuliko yeye aliye katika dunia.”  

Ni kutokana na ushindi aliotupa Yesu Kristo pale msalabani una haki ya kumuambia shetani, magonjwa, dhiki, shida, changamoto kuwa najua umekuja lakini huna kitu kwangu, wachawi hawana madhara kwako, wambeya hawana madhara kwako, wafitini hawana madhara kwako chochote kinachokukabili hapa duniani fahamu amekuja tu lakini hana kitu kwako tembea katika ushindi huu tangu sasa tambua ya kuwa Yesu amekutetea amekufanya kuwa mshindi wa changamoto zozote zinazoendelea hapa duniani usikate tamaa wala usilie unapoteseka wala usimlaani Mungu na kumlaumu na kumuona kama amekuacha wewe tambua tu kuwa kama una Yesu kama una Mungu aliye ndani yako ni mkuu kuliko aliye katika dunia hii sema kila wakati na sema na kila changamoto ya kuwa najua kuwa yu aja mkuu wa ulimwengu huu kwa vyovyote vile hana kitu kwangu katika jina la Yesu Kristo kumbe kama alivyokuwa Yesu hapa ulimwenguni ndivyo tulivyo kwa sababu hiyi shetani hana kitu kwako na kwangu katika jina la Yesu Mwana wa Mungu aliye hai  ameen !        

Na. Rev. Innocent Samuel Kamote

Mkuu wa wajenzi mwenye Hekima

Jumapili, 15 Machi 2026

Akilishika neno la imani vile vile kama alivyofundishwa!


Tito 1:7-9 “Maana imempasa askofu awe mtu asiyeshitakiwa neno, kwa kuwa ni wakili wa MUNGU; asiwe mtu wa kujipendeza nafsi yake, asiwe mwepesi wa hasira, asiwe mlevi wala mgomvi, asiwe mpenda mapato ya aibu.bali awe mkaribishaji, mpenda wema, mwenye kiasi, mwenye haki, mtakatifu, mwenye kudhibiti nafsi yake; akilishika lile neno la imani vile vile kama alivyofundishwa, apate kuweza kuwaonya watu kwa mafundisho yenye uzima, na kuwashinda wenye kupinga.”



Utangulizi:

Mojawapo ya sifa muhimu za viongozi wa kanisa ni pamoja na kuwa waaminifu katika mafundisho sahihi ya imani yetu (Sound Doctrine) na neno la Mungu, Paulo mtume alikuwa amemuacha Tito mtenda kazi pamoja naye katika makanisa yaliyokuwa katika kisiwa cha Krete moja ya kisiwa kikubwa na maarufu sana katika nchi ya Ugiriki, kwa kusudi la kuweka viongozi zamani waliitwa wazee (yaani wachungaji) katika makanisa yaliyokuwako huko.

Tito 1:4-5 “kwa Tito, mwanangu hasa katika imani tuishirikiyo. Neema na iwe kwako na amani zitokazo kwa Mungu Baba na kwa Kristo Yesu Mwokozi wetu. Kwa sababu hii nalikuacha Krete, ili uyatengeneze yaliyopunguka, na kuweka wazee katika kila mji kama vile nilivyokuamuru;”

Hata hivyo katika sifa kadhaa zilizoainishwa na Paulo Mtume kwaajili ya kuchagua viongozi mojawapo ya sifa muhimu sana ilikuwa inahusu kuchagua au kuweka watu ambao watalifundisha neno la Mungu vile vile kama wao walivyofundishwa, hili ilikuwa ni agizo muhimu sana kwa sababu Mafundisho sahihi ni sawa kabisa na mlo kamili wa chakula chenye virutubisho vyote muhimu vinavyohitajika katika mwili wa mwanadamu na mafundisho sahihi vile vile ni ya muhimu katika kanisa la Mungu kwa mustakabali wa kanisa kuwa na Afya njema, ukuaji mzuri wa kiroho, uhakika wa wokovu, na ulinzi wa kanisa dhidi ya mafundisho potofu, kuwanoa waamini, kukuza umoja wa kanisa na kuutunza utakatifu na maisha ya haki kutendeka kwa kazi ya huduma. Kwa msingi huo Kanisa linapochagua watenda kazi, wanafunzi na wenye hekima linapaswa kuhakikisha kuwa watu hao wanateuliwa kwa sababu wameshiba mafundisho yaliyo sahihi na wako tayari kwa huduma na si kwa sababu wana cheo, pesa na heshima fulani huko duniani, kwa Msingi huo leo tutachukua muda kujifunza somo hili muhimu “Akilishika neno la Imani vile vile kama alivyofundishwa!”, na tutajifunza somo hili kwa kuzingatia vipengele vitatu vifuatavyo:-

·         Maana ya kulishika neno la Imani vile vile.

·         Umuhimu wa kulishika neno la Imani vile vile kama ulivyofundishwa.

·         Akilishika neno la Imani vile vile kama alivyofundishwa!,

Maana ya kulishika neno vile vile.

Ni muhimu kufahamu kuwa kulishika neno la Mungu vile vile kama unavyofundishwa maana yake kwa Kiyunani  linatumika neno “antechomenon” au “antechomai” ambalo kwa kiingereza linatumika neno “holding fast to” au “adhering to” au “clinging” au “to hold firm” kwa lugha nzuri ya Kiswahili maana yake ni kushikamana, kung’ang’ania  au kutetea kwa uthabiti, kwa hiyo moja ya sifa ya kiongozi wa kanisa anapaswa kuwa king’ang’anizi, linapokuja swala la kushikamana na Mungu au mafundisho yake hapaswi kuwa mtu unayeyumbishwa, anapaswa kuwa mtu mwenye uwezo wa kusimamia kile unachokiamini kwa nguvu na hakuna mtu wa kukubadilisha.

Ayubu 2:9-10 “Ndipo mkewe akamwambia, Je! Wewe hata sasa washikamana na utimilifu wako? Umkufuru Mungu, ukafe. Lakini yeye akamwambia, Wewe wanena kama mmoja wa hao wanawake wapumbavu anenavyo. Je! Tupate mema mkononi mwa Mungu, nasi tusipate na mabaya? Katika mambo hayo yote Ayubu hakufanya dhambi kwa midomo yake.”

Sifa ya kushikamana na mafundisho ya mitume au injili ya kweli na mafundisho yaliyo sahihi ilikuwa na umuhimu mkubwa sana nyakati za kanisa la kwanza kama ilivyo na umuhimu mkubwa zaidi katika nyakati za leo, kwa hiyo mtu aliyependekezwa kuwa kiongozi alipaswa kuwa na sifa ya kuenenda vile vile kama alivyofundishwa, hakuna uhuru wa kuibadili injili, kwa hiyo kiongozi alikuwa hawezi kupotoshwa wala kuyumbishwa na hawezi kuogopa au kusita kuukemea uwongo, Lengo la kuwafanya wakristo kuwa wanafunzi ni ili wasivutwe kufuata mafundisho ya uongo.

Waefeso 4:11-14 “Naye alitoa wengine kuwa mitume, na wengine kuwa manabii; na wengine kuwa wainjilisti na wengine kuwa wachungaji na waalimu; kwa kusudi la kuwakamilisha watakatifu, hata kazi ya huduma itendeke, hata mwili wa Kristo ujengwe; hata na sisi sote tutakapoufikia umoja wa imani na kumfahamu sana Mwana wa Mungu, hata kuwa mtu mkamilifu, hata kufika kwenye cheo cha kimo cha utimilifu wa Kristo; ili tusiwe tena watoto wachanga, tukitupwa huku na huku, na kuchukuliwa na kila upepo wa elimu, kwa hila ya watu, kwa ujanja, tukizifuata njia za udanganyifu.”

2Timotheo 4:2-4 “lihubiri neno, uwe tayari, wakati ukufaao na wakati usiokufaa, karipia, kemea, na kuonya kwa uvumilivu wote na mafundisho. Maana utakuja wakati watakapoyakataa mafundisho yenye uzima; ila kwa kuzifuata nia zao wenyewe watajipatia waalimu makundi makundi, kwa kuwa wana masikio ya utafiti; nao watajiepusha wasisikie yaliyo kweli, na kuzigeukia hadithi za uongo.”  

Nyakati za kanisa la kwanza walikuwa makini sana kuhakikisha kuwa mtu wanayemkaribisha anakuwa na imani ile ile iliyofundishwa na kukubalika na mitume, Mitume waliagiza kuwa hakukuwa na sababu ya kumchekea mtu ambaye hakai au haleti mafundisho yao, walikazia kuwa mtu wa namna hiyo ikiwezekana wasimkaribishe wala hata wasimsalimie, mwenye dhambi anaweza kubadilika hata pole pole, lakini mafundisho ya uongo hata salamu asipewe

2Yohana 1:8-11 “Jiangalieni nafsi zenu msiyapoteze mliyoyatenda, bali mpokee thawabu timilifu. Kila apitaye cheo, wala asidumu katika mafundisho ya Kristo, yeye hana Mungu. Yeye adumuye katika mafundisho hayo, huyo ana Baba na Mwana pia. Mtu akija kwenu, naye haleti mafundisho hayo, msimkaribishe nyumbani mwenu, wala msimpe salamu. Maana yeye ampaye salamu azishiriki kazi zake mbovu.”

Kanisa linapaswa kusimamia msimamo huu, kuhakikisha kuwa kila mtu anayekaribishwa katika kanisa letu anakuja na fundisho lililo sahihi, anakuja na msimamo ule ule waliokuwa nao mitume wa Bwana wetu Yesu Kristo, au mtu anayechaguliwa kuwa kiongozi katika kanisa analishika neno la imani vile vile kama tulivyofundishwa na sio vinginevyo, mafundisho ya mitume yanapaswa kushikiliwa kama mila na desturi ya kanisa na kurithishwa katika kizazi kinachokuja hata akifufuka Paulo mtume leo atatukuta tukihubiri injili ile ile aliyoiacha na atatukuta hatujaichakachua injili wala hatuhubiri injili nyingine, na tutakemea kwa Mamlaka yote, kuonya na kukaripia. Kwa mafundisho yenye uzima. Haiwezekani Leo kiongozi mkubwa kabisa wa imani hatambui utatu na anachekewa

Umuhimu wa kulishika neno la imani vile vile kama ulivyofundishwa

Ni muhimu kufahamu kuwa mitume walikuwa wakali sana na swala zima la mfundisho ya uwongo kuliko tunavyofikiri, kwa bahati mbaya makanisa mengi leo wamekuwa wakali kwa dhambi jambo ambalo sio baya, kuliko kwa mafundisho potofu, dhambi inaweza kutubiwa na mwenye dhambi anaweza kubadilika, ukuaji wa kiroho ni mchakato na sio jambo la hatari kwa kanisa kwa sabahu Kristo alikuja kuokoa, lakini mafundisho potofu ni chachu na inaweza kubadilisha na kuathiri muelekeo mzima wa mwili wa Kristo na kwa sababu hiyo mitume walikuwa wakali sana na watu wanaofundisha uongo, Paulo mtume anamwagiza Tito kuwa makini kuwachagua watu wenye msimamo katika mafundisho yetu kwa sababu kisiwa cha Krete kilikuwa ni miongoni mwa sehemu zilizoathiriwa na mafundisho ya uongo kwa hiyo waliopendekezwa kuchaguliwa kuwa viongozi walipaswa kuwa watu hodari ambao wanauwezo wa kufundisha, kukemea, kuonya  na kuwazidi wale wanaowapinga au wale wanaoipinga kweli

Tito 1:4-5 “kwa Tito, mwanangu hasa katika imani tuishirikiyo. Neema na iwe kwako na amani zitokazo kwa Mungu Baba na kwa Kristo Yesu Mwokozi wetu. Kwa sababu hii nalikuacha Krete, ili uyatengeneze yaliyopunguka, na kuweka wazee katika kila mji kama vile nilivyokuamuru;”

Tito 1:7-9 “Maana imempasa askofu awe mtu asiyeshitakiwa neno, kwa kuwa ni wakili wa MUNGU; asiwe mtu wa kujipendeza nafsi yake, asiwe mwepesi wa hasira, asiwe mlevi wala mgomvi, asiwe mpenda mapato ya aibu.bali awe mkaribishaji, mpenda wema, mwenye kiasi, mwenye haki, mtakatifu, mwenye kudhibiti nafsi yake; AKILISHIKA LILE NENO LA IMANI VILE VILE KAMA ALIVYOFUNDISHWA, apate kuweza kuwaonya watu kwa mafundisho yenye uzima, na kuwashinda wenye kupinga.”

Kulikuwa na walimu wa uongo kule Krete, watu walikazia sheria ya Musa na mafundisho ya tohara, na pia watu walijitafutia mapato kupitia dini, kwa sababu hiyo suluhisho halikuwa miujiza bali suluhisho lilikuwa ni kupata watu sahihi watakaosimamia misingi ya Imani ya mitume na kuifundisha vile vile kama walivyofundishwa na wenye sifa ya kuweza kung’amua na kuyapinga au kuwashinda wale wenye kupinga kama alivyokuwa mtu wa Mungu Stefano, Paulo alikuwa anataka viongozi wawe wakali kwenye fundisho sahihi wenye sifa za ugumu wa kusimamia Imani na kupinga mafundisho ya uongo na kuwakemea waongo kwa nguvu zao zote, watu wenye uwezo wa kuwashinda wapingao na kuisimamia Imani kwa uaminifu hata kaa itawagharimu kufa 

Tito 1:10-14 “Kwa maana kuna wengi wasiotii, wenye maneno yasiyo na maana, wadanganyaji, na hasa wale wa tohara, ambao yapasa wazibwe vinywa vyao. Hao wanapindua watu wa nyumba nzima, wakifundisha yasiyowapasa kwa ajili ya mapato ya aibu. Mtu wa kwao, nabii wao wenyewe, amesema, Wakrete ni waongo siku zote, hayawani wabaya, walafi wavivu. Ushuhuda huo ni kweli. Kwa sababu hiyo uwakemee kwa ukali, ili wapate kuwa wazima katika imani; wasisikilize hadithi za Kiyahudi, wala maagizo ya watu wajiepushao na yaliyo kweli.”

Matendo 6:8-10 “Na Stefano, akijaa neema na uwezo, alikuwa akifanya maajabu na ishara kubwa katika watu. Lakini baadhi ya watu wa sinagogi lililoitwa sinagogi la Mahuru, na la Wakirene, na la Waiskanderia, na la wale wa Kilikia na Asia, wakaondoka na kujadiliana na Stefano;lakini hawakuweza kushindana na hiyo hekima na huyo Roho aliyesema naye.”

Kanisa linapaswa kuwa makini kuhakikisha kuwa linasimamisha watu waliojaa neno la Mungu, watu wenye injili iliyosahihi, watu wanaofunzwa vizuri ili kuirithisha Imani iliyosahihi kwa kizazi kinachokuja, leo hii kumejaa upuuzi wa kila aina kila kona kwa sababu ya uzembe wa Kanisa, Kanisa linafukuzana na mambo mengine na linaacha kuwafanya watu kuwa wanafunzi wa neno la Mungu, ni lazima tuikabidhi injili kwa watu waaminifu watakaofaa kuwafundisha na wengine vile vile kama walivyofundishwa, dunia ikijawa na mafundisho ya uongo leo sababu kubwa ni uzembe wa Kanisa kutokuwafundisha watu neno la Mungu, Kanisa ni lazima liwe kama shule ukiachanana maombezi na miujiza ambayo nayo ni ya muhimu lakini bila kusahau kuwafundisha watu neno, watu ni lazima wajae neno, dunia ni lazima ijawe na mafundisho yetu mpaka wakuu wa dini pinzani walalamike kama ilivyotokea kwa Masadukayo. 

2Timotheo 2:2 “Na mambo yale uliyoyasikia kwangu mbele ya mashahidi wengi, hayo uwakabidhi watu waaminifu watakaofaa kuwafundisha na wengine.”

Matendo 5:27-29 “Walipowaleta, wakawaweka katika baraza. Kuhani Mkuu akawauliza, akisema, Je! Hatukuwaamuru ninyi kwa nguvu, msifundishe kwa jina hili? Nanyi, tazameni, mmeijaza Yerusalemu mafundisho yenu, na mnataka kuileta damu ya mtu yule juu yetu. Petro na mitume wakajibu, wakisema, Imetupasa kumtii Mungu kuliko wanadamu.”

Kila kanisa ambalo linaamini kuwa lina mafundisho ya kweli basi lina wajibu wa kuijaza dunia na mafundisho hayo ya kweli kwa kuihubiri injili kila mahali, kufanya wanafunzi na kuijaza dunia na mafundisho yetu, kama hatufanyi kazi hiyo itafanywa kwa uaminifu na mashahidi wa Yehova, Mormonisim, Wasabato, na imani nyinginezo nyingi, injili za mafanikio, injili za neema iliyozidi, injili za sheria, na injili nyingine nyingi na usikasirike wakiwa na televisheni, magazeti na washuhudiaji wanapita nyumba kwa nyumba wakieneza mafundisho yao maana wewe hutaki na mafundisho yako lakini pembeni pembeni unadai una Imani ya kweli lakini umekaa nayo kimya na kazi yako ni kukosoa tu pembeni utasikia jihadharini na mafundisho ya mitandaoni, ahaaaa we ya kwako ya mitandaoni yako wapi na kwa nini hurushi? Kwa hiyo wadhani Kristo hana wanaohubiri kweli mitandaoni? Mwone kwanza lihubiri neno fundisha kweli eneza kweli kwa njia zozote, wafundishe washirika kupambanua mchele na chuya!   

Akilishika neno la Imani vile vile kama alivyofundishwa!.

Unadhani kuna faida gani ya kuwa na umati mkubwa wa watu, kuwa na sauti nzuri, kuwa na karama za kila aina, kutajirika na kubarikiwa sana na kuwa na walinzi na msafara wa magari lakini ukawa hauifundishi kweli? Kiongozi wa kweli wa imani ni lazima awe mwanafunzi mzuri wa neno la Mungu, awe mtetezi wa kweli wa imani, awe na uwezo wa kung’amua uongo na kuukemea kwa nguvu na kuukaripia au kuujibu kwa neno la Mungu, lakini zaidi sana awe mwaminifu kwa mafundisho ya mitume, na sio kwa sababu umerithi tu bali pia kwa sababu umelichunguza na kujithibitishia kuwa unaamini jambo lililo sahihi, mmesikia siku za Karibuni katika mitandao wahubiri wakubwa kabisa wenye umati mkubwa wa watu wakikanusha na kuushambulia na kupinga fundisho la utatu wa Mungu na watu wenye kweli wamekaa kimya tu hii ni mojawapo ya hatari iliyo wazi kuwa nyakati za leo tuna watu wengi tu wanaofuata mkumbo, kama watu wangekuwa wanafundishwa kweli ya Mungu kwa usahihi  na wakawa na uwezo mkubwa wa kupambanua nadhani siku ile wanamsikia kiongozi wao akisema hakuna Utatu ingekuwa ndio siku ya mwisho kuabudu hapo, lakini dunia imejaa vipofu, na viongozi wa vipofu, wala hawaoni kuwa hili ni tatizo kubwa!.

Kama kanisa tangu mwanzo lingezalisha watu wasioyumbishwa, imani yetu ingebaki kama ilivyokuwa nyakati za baba zetu, lakini siku za leo kumejaa nyumbu wengi makanisani ambao wanayumbishwa kila kukicha na Imani mbalimbali na imekuwa ngumu kwao leo kujua ipi ni sahihi na ipi ni potofu watu hawajui kupambanua. Mtu anayeishika Imani vile vile ni mtu asiyetikisika kwa sababu anajua alichokiamini na hawatikiswi na lolote wanashikamana na kile walichokiamini bila kujali wanapitia nini

-          2Timotheo 1:12-14 “Kwa sababu hiyo nimepatikana na mateso haya, wala sitahayari; kwa maana namjua yeye niliyemwamini, na kusadiki ya kwamba aweza kukilinda kile nilichokiweka amana kwake hata siku ile. Shika kielelezo cha maneno yenye uzima uliyoyasikia kwangu, katika imani na upendo ulio katika Kristo Yesu. Ilinde ile amana nzuri kwa Roho Mtakatifu akaaye ndani yetu.”

 

-          Matendo 5:27-29. “Walipowaleta, wakawaweka katika baraza. Kuhani Mkuu akawauliza, akisema, Je! Hatukuwaamuru ninyi kwa nguvu, msifundishe kwa jina hili? Nanyi, tazameni, mmeijaza Yerusalemu mafundisho yenu, na mnataka kuileta damu ya mtu yule juu yetu. Petro na mitume wakajibu, wakisema, Imetupasa kumtii Mungu kuliko wanadamu.”

 

Kanisa ni lazima tujikite katika kuandaa viongozi ambao watakuwa watata, wenye kumfuata Yesu na kukataa kuyachakachua maneno ya Mungu kwa gharama yoyote hata kama itawagharimu kuteseka na kuuawa, lazima tuzalishe viongozi mahiri wenye uwezo wa kumuigiza Yesu, kuwa hatukuja duniani kuwapendeza wanadamu bali tumekuja kuwatumikia watu kama yeye mwenyewe, lazima tuzalishe watu wenye nguvu, wenye akili wanaolijua neno ambao watasimama kuitetea Imani hata wakati wa mambo magumu na kuwasaidia watu kuijua kweli na kuisimamimai kwa gharama yoyote kwa sababu hiyo pamoja na sifa nyingine isisahahulike sifa hii muhimu ya kwamba imempasa askofu au kiongozi wa kanisa awe mtu anayeisimamia Imani vile vile kama alivyofundishwa .

Tito 1:7-9 “Maana imempasa askofu awe mtu asiyeshitakiwa neno, kwa kuwa ni wakili wa MUNGU; asiwe mtu wa kujipendeza nafsi yake, asiwe mwepesi wa hasira, asiwe mlevi wala mgomvi, asiwe mpenda mapato ya aibu.bali awe mkaribishaji, mpenda wema, mwenye kiasi, mwenye haki, mtakatifu, mwenye kudhibiti nafsi yake; akilishika lile neno la imani vile vile kama alivyofundishwa, apate kuweza kuwaonya watu kwa mafundisho yenye uzima, na kuwashinda wenye kupinga.”

Na. Rev. Innocent Samuel Kamote

Mkuu wa wajenzi mqwenye Hekima