Jumapili, 28 Juni 2026

Mwenende kama ulivyo wajibu wenu kwa Bwana!


Wakolosai 1:9-11 “Kwa sababu hiyo sisi nasi, tangu siku ile tuliposikia, hatuachi kufanya maombi na dua kwa ajili yenu, ili mjazwe maarifa ya mapenzi yake katika hekima yote na ufahamu wa rohoni; MWENENDE KAMA ULIVYO WAJIBU WENU KWA BWANA, mkimpendeza kabisa; mkizaa matunda kwa kila kazi njema, na kuzidi katika maarifa ya Mungu; mkiwezeshwa kwa uwezo wote, kwa kadiri ya nguvu ya utukufu wake, mpate kuwa na saburi ya kila namna na uvumilivu pamoja na furaha; mkimshukuru Baba, aliyewastahilisha kupokea sehemu ya urithi wa watakatifu katika nuru.”

 



Utangulizi:

Ni muhimu kufahamu kuwa mara baada ya kuwa tumeokolewa kwa neema ya Mungu, kwa njia ya imani, tunapaswa sana kuzingatia mwenendo wetu, Mtu aliyeokoka hataishi maisha anayojitakia tu kwa sababu ameokolewa, Lakini maandiko yanatoa maelekezo ya jinsi tunavyopaswa kuishi, yaani uko wajibu wetu tunaopaswa kutembea katika huo ili tuweze kuwa mfano wa kuigwa kama wana wa Mungu tuwapo hapa ulimwenguni, mwenendo huo ni wa lazima na wala sio wa hiyari, tunapaswa kuendenda kama vile Yesu Kristo mwenyewe alivyoenenda hapa duniani.

 

1Yohana 2:4-6 “Yeye asemaye, Nimemjua, wala hazishiki amri zake, ni mwongo, wala kweli haimo ndani yake. Lakini yeye alishikaye neno lake, katika huyo upendo wa Mungu umekamilika kweli kweli. Katika hili twajua ya kuwa tumo ndani yake. Yeye asemaye ya kuwa anakaa ndani yake, imempasa KUENENDA mwenyewe vile vile kama yeye ALIVYOENENDA.”

 

Katika maandiko yetu ya Msingi Paulo mtume anawaandikia Wakolosai aina ya maombi anayowaombea na kuwalekeza watu hao wajazwe maarifa ya mapenzi yake katika hekima yote na ufahamu wa rohoni ili kwamba waenende kama ulivyo wajibu wao kwa Bwana wakimpendeza yeye Kabisa!, Kumbe tunagundua ya kuwa kuna namna basi Wakristo tunapaswa kuenenda na swala hili liko wazi kabisa katika neno la Mungu. Kuna namna ya kutembea katika ulimwengu huu

 

Wafilipi 2:14-15 “Yatendeni mambo yote pasipo manung'uniko wala mashindano, mpate kuwa wana wa Mungu wasio na lawama, wala udanganyifu, wasio na ila kati ya kizazi chenye ukaidi, kilichopotoka; ambao kati ya hao mnaonekana kuwa kama mianga katika ulimwengu,”

 

Tito 2:11-12 “Maana neema ya Mungu iwaokoayo wanadamu wote imefunuliwa; nayo yatufundisha kukataa ubaya na tamaa za kidunia; tupate kuishi kwa kiasi, na haki, na utauwa, katika ulimwengu huu wa sasa;

 

Wakolosai 2:4-6 “Nasema neno hili, mtu asije akawadanganya kwa maneno ya kuwashawishi. Maana nijapokuwa sipo kwa mwili, lakini nipo pamoja nanyi kwa roho, nikifurahi na kuuona utaratibu wenu na uthabiti wa imani yenu katika Kristo. Basi kama mlivyompokea Kristo Yesu, Bwana, ENENDENI vivyo hivyo katika yeye;”

 

Kwa msingi huo utaweza kuona kuwa maandiko matakatifu yana namna ambayo kwamba Roho Mtakatifu ametukusudia sisi kuenenda sawasawa na maelekezo yanayotolewa katika maandiko lakini ili tuweze kuendelea kuelewa vizuri hatuna budi kufahamu maswala kadhaa ikiwa ni pamoja na maana ya neno mwenendo, tutajifunza somo hili Mwenende kama ulivyo wajibu wenu kwa Bwana! Kwa kuzingatia vipengele muhimu vitatu vifuatavyo;-

 

·         Maana ya neno mwenendo.

·         Jinsi inavyotupasa kuenenda.

·         Mwenende kama ulivyo wajibu wenu kwa Bwana!

 

Maana ya neno mwenendo.

 

Neno mwenendo ambalo limejitokeza zaidi ya mara 13 katika maandiko ya Kiyunani linasomeka kama “AnastrophÄ“” ambalo katika Biblia ya kiingereza linasomeka kama “conversation”, au “Behavior” au “Conducts” Katika Biblia ya Kiswahili limetumika neno mawazo, au mtazamo, tabia au mwenendo  kwa mfano kabla ya kuokoka mtu anaweza kuwa na tabia au mwenendo  ua mawazo yanayomuongoza kuwa na tabia hiyo, kwa hiyo mwenendo ni jumla ya mtazamo wa mtu na mazingira yanayopelekea awe na tabia hiyo aliyo nayo, Paulo mtume kabla ya kuokoka alikuwa na mtazamo kuwa Ukristo sio imani ya kweli na kwa sababu hiyo aliwatesa sana Wakristo na kanisa la kwanza kwa sababu mtazamo wake ulipelekea kuwa na mwenendo au tabia aliyokuwa nayo kabla ya kukutana na Bwana Yesu.

 

Wagalatia 1:13Maana mmesikia habari za MWENENDO wangu zamani katika dini ya Kiyahudi, kwamba naliliudhi kanisa la Mungu kupita kiasi, nikaliharibu. Nami naliendelea katika dini ya Kiyahudi kuliko wengi walio hirimu zangu katika kabila yangu, nikajitahidi sana katika kuyashika mapokeo ya baba zangu. Lakini Mungu, aliyenitenga tangu tumboni mwa mama yangu, akaniita kwa neema yake,”

 

Kwa hiyo mtu aliyeokoka anapaswa kuwa na mabadiliko ya mwenendo wake wa kwanza au ule wa zamani na anapaswa kuvaa mwenendo mpya unaotembea katika hali ya uchaji wa Mungu kwa kuzingatia kweli, haki na utakatifu, kwa sababu hiyo mtu aliyemwamini Bwana anatarajiwa awe na mwenendo tofauti na ule aliokuwa akiuendea zamani, haya ni mabadiliko yanayoanzia kwemye mtazamo, fundisho na kuonekana katika tabia na mtazamo mpya unaompa Mungu utukufu baada ya kumpokea Yesu kama Bwana na mwokozi wa maisha yetu!

 

Waefeso 4:20-24 “Bali ninyi, sivyo mlivyojifunza Kristo; ikiwa mlimsikia mkafundishwa katika yeye, kama kweli ilivyo katika Yesu, mvue kwa habari ya MWENENDO wa kwanza utu wa zamani, unaoharibika kwa kuzifuata tamaa zenye kudanganya; na mfanywe wapya katika roho ya nia zenu; mkavae utu mpya, ulioumbwa kwa namna ya Mungu katika haki na utakatifu wa kweli.”

 

Jinsi inavyotupasa kuenenda.

 

Tumejifunza sasa maana ya mwenendo na tumeona jinsi maandiko yanavyotuelezea kuwa uko mwenendo ambao tuliuendea zamani kabla ya kuokolewa na sasa baada ya kuwa tumeokolewa kuna aina ya mwenendo ambao tunapaswa kuuenenda na bila kufundishwa wakati mwingine inaweza kuwa ngumu kwetu kujua ni mwenendo gani tunapaswa kuufuata? Kwa hiyo yako mambo kadhaa ambayo Biblia inatuasa kuyafuata au kuyajifunza ili yaweze kuwa dira na njia ya kuujenga mwenendo wetu na huo ndio wajibu wetu ambao umesisitizwa katika maandiko ya msingi kwamba Mwenende kama ulivyo wajibu wenu kwa Bwana ni wajibu upi huo hapa yako mambo kadhaa ya kuyaangalia

 

1.       Ni wajibu wetu kuenenda kwa utakatifu – Utakatifu ni moja ya mwenendo ambao watu waliookoka wanapaswa kuwa nao, ni muhimu kuelewa kuwa ni vigumu kumuona Mungu bila ya kuwa na mwenendo wa utakatifu, utakatifu ni nini hasa? Biblia ya Kiyunani inatumia neno “Hagio” ambalo ni sawa na neno la Kiingereza “Pure morally” au “Blameless  maana yake kuendenda kwa uadilifu, au kutembea bila lawama, wakati wote katika maisha yetu isitokee tumelaumiwa kama watu wabaya au kwa kutenda mambo yasiyo ya uadilifu

 

1Petro 1:14-16. “Kama watoto wa kutii msijifananishe na tamaa zenu za kwanza za ujinga wenu; bali kama yeye aliyewaita alivyo mtakatifu, ninyi nanyi iweni watakatifu katika MWENENDO wenu wote; kwa maana imeandikwa, Mtakuwa watakatifu kwa kuwa mimi ni mtakatifu.”

 

2.       Ni wajibu wetu kuendenda kwa imani – watu wa Mungu wanapaswa kuenenda kwa Imani, pasipo imani haiwezekani kumpendeza Mungu, kwa hiyo yote tuyatendayo tunapaswa kuyafanya kwa imani, Mungu aliwaangamiza wana wa Israel wengi jangwani kwa sababu ya kutokuamini kwao, tukiendenda kwa imani ni rahisi kumpendeza Mungu, watu wa Mungu wanapaswa kuliamini neno la Mungu na kulitii kwa imani na sio kwa kutegemea yale tuyaonayo kwa macho ya kibinadamu au mazingira yanayokuzunguka

 

2Wakorintho 5:6-8 “Basi siku zote tuna moyo mkuu; tena twajua ya kuwa, wakati tuwapo hapa katika mwili, tunakaa mbali na Bwana. (Maana TWAENENDA kwa imani, si kwa kuona.) Lakini tuna moyo mkuu; nasi tunaona ni afadhali kutokuwamo katika mwili na kukaa pamoja na Bwana.”

 

3.       Ni wajibu wetu kuenenda kwa Upendo – Kuenenda kwa upendo ni mojawapo ya agizo la watu wa Mungu, kuishi kwa upendo, kutembea kwa upendo kujawa na upendo maisha yetu ni lazima yaonyeshe upendo wa kujitoa kama vile Kristo alivyojitoa kwetu na kwa ulimwengu ili kila amuaminiye aokolewe, chuki, husuda na wivu, magombano, visasi na majungu kamwe sio mwenendo wanaopaswa kuwa nao watu ambao Kristo amewafia Msalabani kwa kujitoa kuliko kukuu hata tulipokuwa wenye dhambi

 

Waefeso 5:1-2 “Hivyo mfuateni Mungu, kama watoto wanaopendwa; MKAENENDE katika upendo, kama Kristo naye alivyowapenda ninyi tena akajitoa kwa ajili yetu, sadaka na dhabihu kwa Mungu, kuwa harufu ya manukato.”

 

4.       Ni wajibu wetu kuenenda nuruni – Kuenenda nuruni kwa ufupi maana yake ni kutembea kwa kuweka kipaumbele maswala na maagizo ya Mungu, Mungu ni Nuru, Yesu Kristo mwenyewe pia alisema yeye ni Nuru ya ulimwengu, kwa sababu hiyo tunapoweka kipaumbele maswala Yote ambayo Yesu Kristo ametufundisha na kumfuata, maana yake tunaendenda Nuruni, kwenda kinyume na maagizo ya neno la Mungu ni kuenenda gizani

 

1Yohana 1:5-7 “Na hii ndiyo habari tuliyoisikia kwake, na kuihubiri kwenu, ya kwamba Mungu ni nuru, wala giza lo lote hamna ndani yake.Tukisema ya kwamba twashirikiana naye, tena tukienenda gizani, twasema uongo, wala hatuifanyi iliyo kweli; bali TUKIENENDA NURUNI, kama yeye alivyo katika nuru, twashirikiana sisi kwa sisi, na damu yake Yesu, Mwana wake, yatusafisha dhambi yote.”

 

5.       Ni wajibu wetu kuenenda katika upya wa maisha – kutembea katika upya wa maisha kunamaanisha ni lazima maisha yetu yabadilike tuwe na mwenendo mpya na sio ule wa zamani, kabala ya kuokolewa, hatupaswi tena kuitumikia dhambi ambayo tuliiendea zamani kabla ya kukutana na Yesu, sasa kwa kuwa tumekutana na Yesu hatuna budi kuenenda katika upya huu wa maisha na kutembea na Mungu, uongo, ulevi, tamaa mbaya, uchafu, kiburi, masengenyo, ubinafsi na kujihesabia haki pamoja na maovu ya kila namna hayapaswi kuonekana tena kwa mtu anayewajibika kuenenda katika upya wa maisha

 

Warumi 6:4-6 “Basi tulizikwa pamoja naye kwa njia ya ubatizo katika mauti yake, kusudi kama Kristo alivyofufuka katika wafu kwa njia ya utukufu wa Baba, vivyo hivyo na sisi TUENENDE KATIKA UPYA WA UZIMA. Kwa maana kama mlivyounganika naye katika mfano wa mauti yake, kadhalika mtaunganika kwa mfano wa kufufuka kwake; mkijua neno hili, ya kuwa utu wetu wa kale ulisulibishwa pamoja naye, ili mwili wa dhambi ubatilike, tusitumikie dhambi tena;”

 

6.       Ni wajibu wetu kuenenda kwa Roho – kuenenda kwa Roho maana yake ni nini? Ni maisha ambayo Roho Mtakatifu ndiye anayetawala, kila mtu aliyeokolewa ni muhimu na lazima atoe nafasi na kumruhusu Roho Mtakatifu kuyaongoza na kuyatawala maisha yake katika kila nyanja ya maisha na kumruhusu yeye kutusaidia kukomaa kiroho na kuzaa matunda ya Roho Mtakatifu katika maisha yetu, maisha yako unayaongoza wewe mwenyewe au unamuachia Roho akuongoze? Kuenenda kwa roho ni kumuachia yeye atuongoze maisha yetu.

 

Wagalatia 5:16-23 “Basi nasema, ENENDENI kwa Roho, wala hamtazitimiza kamwe tamaa za mwili. Kwa sababu mwili hutamani ukishindana na Roho, na Roho kushindana na mwili; kwa maana hizi zimepingana, hata hamwezi kufanya mnayotaka. Lakini mkiongozwa na Roho, hampo chini ya sheria. Basi matendo ya mwili ni dhahiri, ndiyo haya, uasherati, uchafu, ufisadi, ibada ya sanamu, uchawi, uadui, ugomvi, wivu, hasira, fitina, faraka, uzushi, husuda, ulevi, ulafi, na mambo yanayofanana na hayo, katika hayo nawaambia mapema, kama nilivyokwisha kuwaambia, ya kwamba watu watendao mambo ya jinsi hiyo hawataurithi ufalme wa Mungu. Lakini tunda la Roho ni upendo, furaha, amani, uvumilivu, utu wema, fadhili, uaminifu, upole, kiasi; juu ya mambo kama hayo hakuna sheria.”

 

7.       Ni wajibu wetu kuenenda kama unavyostahili wito wetu – Kila mtu aliyeokolewa kuna namna Mungu amemuita amtumikie katika mazingira mbalimbali na huo ndio wito wako, hapa wito haimaanishi ule wito wa kumtumikia Mungu pekee, wito maalumu, unaweza kuwa Mwalimu, Polisi, Daktrari, Mtoza ushuru, Mwanasiasa na kadhalika Mungu anataka uwe na mwenendo mwema katika kila aina ya wito ulioitiwa au kokote kule unakokuweko hata kama wewe ni fundi cherehani, iko miiko ya utumishi katika kile eneo la wito wa maisha basi huko enenda kama unavyoustahili wito wako, zaidi sana katika nyumba ya Mungu  huku tukitunza amani.

 

Waefeso 4:1-3 Kwa hiyo nawasihi, mimi niliye mfungwa katika Bwana, MWENENDE kama inavyoustahili wito wenu mlioitiwa; kwa unyenyekevu wote na upole, kwa uvumilivu, mkichukuliana katika upendo; na kujitahidi kuuhifadhi umoja wa Roho katika kifungo cha amani.”

 

8.       Ni wajibu wetu kuenenda kwa Hekima – Ni kama maandiko yanatuambaia wazi kuwa muda wetu duniani sio wa kwetu ni muda wa Mungu, Ni muda ambao tumepewa kwa kusudi la kumtumikia Mungu na kutimiza kusudi lake au mapenzi yake kwa hiyo Muda ni wa maana sana kwa watu waliookoka na haupaswi kupotezwa bure, watu wanaopoteza muda wanaitwa wasio na hekima au wajinga, ni lazima tujiangalie tunautumiaje Muda hasa sisi waafrika, tunaweza kutumia muda mwingi sana kupiga soga ua kusengenya muda ambao tungeweza kuutumia kwaajili ya Mungu, kwa kuyajua mapenzi yake na kuyafanya

 

Waefeso 5:15-17 “Basi angalieni sana jinsi MNAVYOENENDA; si kama watu wasio na hekima bali kama watu wenye hekima; mkiukomboa wakati kwa maana zamani hizi ni za uovu. Kwa sababu hiyo msiwe wajinga, bali mfahamu ni nini yaliyo mapenzi ya Bwana.”

 

9.       Ni wajibu wetu kuenenda vilevile kama tulivyompokea Kristo – Kuenenda vile vile kama tulivyompokea Kristo hakumaanishi ubaki vilevile baada ya kuokoka, lakini maana yake kila siku tunapaswa kuishi vile vile sawasawa na mafundisho tunayoyapokea kwa Bwana wetu Yesu Kristo kupitia Mwalimu wa Kweli Roho Mtakatifu, huku ni kuendelea kudumisha uhusiano wetu na Mungu kwa kutii na kujileta katika neema yake kukua katika upendo, unyenyekevu na hekima na kuhakikisha kuwa haturudi nyuma tangu tulipoanza uhusiano wetu na yeye.

 

Wakolosai 2:6-7 “Basi kama mlivyompokea Kristo Yesu, Bwana, ENENDENI vivyo hivyo katika yeye; wenye shina na wenye kujengwa katika yeye; mmefanywa imara kwa imani, kama mlivyofundishwa; mkizidi kutoa shukrani.

 

10.   Ni wajibu wetu kuenenda kwa kuikulia neema – Tumeokolewa kwa neema sisi kama wana wa Mungu ni wana wa neema kwa msingi huo hatuna budi kukua kwa kuikulia neema ya Mungu ni neema ya Mungu ndiyo inayotusaidia katika, kuukulia wokovu na kukomaa kiroho kwa hiyo hatuna budi kujitoa sisi wenyewe na kuenenda kwa kuikulia neema kwa kuendelea kutenda mema

 

Waefeso 2:8-10 “Kwa maana mmeokolewa kwa neema, kwa njia ya imani; ambayo hiyo haikutokana na nafsi zenu, ni kipawa cha Mungu; wala si kwa matendo, mtu awaye yote asije akajisifu. Maana tu kazi yake, tuliumbwa katika Kristo Yesu, tutende matendo mema, ambayo tokea awali Mungu aliyatengeneza ili TUENENDE NAYO.”

 

Mwenende kama ulivyo wajibu wenu kwa Bwana!

 

Wokovu ni Msaada wa Mungu kwetu, hata hivyo tabia na mwenendo ni wajibu wetu na ndio maana neno la Mungu linasema mwenende kama ulivyo wajibu wenu kwa Bwana, ni wajibu wetu kujitoa kwa Mungu na kukubali neema ya Mungu ituendeshe katika maisha haya kama watoto wake uili tuweze kuwa na mvuto hapa ulimwenguni, mwenendo wetu una nafasi kubwa mbili, kuimarisha uhusiano wetu wa ndani na Mungu, na pili kuwavutia wengine au kuwafundisha kivitendo jinsi Mungu alivyo mwadilifu, kuenenda kama ulivyo wajibu wetu kwa Bwana kumpa Mungu heshima inayoonyesha kuwa Mungu anabadilisha  maisha ya watu wake, tunaweza kuitangaza injili hata bila kusema neno kupitia tu mwenendo mwema, aina binadamu wote duniani wanajua kiwango cha uadilifu ambao watu wa Mungu wanapaswa kuenenda na ndio maana ukifanya mambo ya ajabu wanajua, kutokana na umuhimu wa jambo hili Paulo mtume aliwaombea sana wakolosai wajazwe maarifa, na hekima na ufahamu wa rohoni ili waenende kama ulivyo wajibu wao kwa Bwana wakimpendeza kabisa sio hivyo tu wakiwavutia watu wengine wasioamini waweze kuokolewa ili hayo yatimie hatuna budi kujitoa na kuhakikisha vile vile tunajileta wenyewe kanisani katika ibada za mafundisho ili tukutane na neno la Mungu litakalotupoa hekima na maarifa ili tujue nemna inavyotupasa kuenenda

 

Wakolosai 1:9-11 “Kwa sababu hiyo sisi nasi, tangu siku ile tuliposikia, hatuachi kufanya maombi na dua kwa ajili yenu, ili mjazwe maarifa ya mapenzi yake katika hekima yote na ufahamu wa rohoni; MWENENDE KAMA ULIVYO WAJIBU WENU KWA BWANA, mkimpendeza kabisa; mkizaa matunda kwa kila kazi njema, na kuzidi katika maarifa ya Mungu; mkiwezeshwa kwa uwezo wote, kwa kadiri ya nguvu ya utukufu wake, mpate kuwa na saburi ya kila namna na uvumilivu pamoja na furaha; mkimshukuru Baba, aliyewastahilisha kupokea sehemu ya urithi wa watakatifu katika nuru.”

 

1Petro 3:1-2 “Kadhalika ninyi wake, watiini waume zenu; kusudi, ikiwa wako wasioliamini Neno, wavutwe kwa MWENENDO wa wake zao, pasipo lile Neno; wakiutazama MWENENDO wenu safi, na wa hofu.”

 

Mwenendo ni msingi muhimu sana katika maisha ya Ukristo, ni lazima kila Mkristo awe na mwenendo unaomuakisi Yesu Kristo na hii ni kanuni Muhimu sana katika maisha ya ukristo na mwenendo wa kibiblia, mwenendo mwema mbele ya watu wasiomjua Mungu huwavutia watu wengine wapate kuokolewa, na sio hivyo tu ni mwenendo ndio unaotusaidia kupata viongozi wa kanisa ambao mfano wao unaweza kuigizwa na wengine mwenendo unatajwa kama hekima na tabia nzuri, unatajwa kama utetezi tunaposingiziwa, unaonyesha kielelelzo kama viongozi katika nyumba ya Mungu kwa hivyo tukiwajibika vizuri kwa Bwana tutawavutia watu kukubali ukweli ya kuwa Mungu anaokoa na anabadilisha watu wake kwa sababu watu wataona mabadiliko makubwa ya mwenendo wetu.

 

Yakobo 3:11-13. “Je! Chemchemi katika jicho moja hutoa maji matamu na maji machungu? Ndugu zangu, Je! Mtini waweza kuzaa zeituni, au mzabibu kuzaa tini? Kadhalika chemchemi haiwezi kutoa maji ya chumvi na maji matamu. N'nani aliye na hekima na ufahamu kwenu? Na aonyeshe kazi zake kwa MWENENDO wake mzuri, katika upole wa hekima.”

 

1Timotheo 4:12 “Mtu awaye yote asiudharau ujana wako, bali uwe kielelezo kwao waaminio, katika usemi na MWENENDO, na katika upendo na imani na usafi.”

 

1Petro 2:12 “Mwe na MWENENDO mzuri kati ya Mataifa, ili, iwapo huwasingizia kuwa watenda mabaya, wayatazamapo matendo yenu mazuri, wamtukuze Mungu siku ya kujiliwa.”

 

Na Rev. Innocent Samuel Kamote

 

Mkuu wa wajenzi mwenye Hekima

Jumapili, 21 Juni 2026

Kumbe ni Lea badala ya Raheli!


Mwanzo 29:20-26 “Yakobo akatumika miaka saba kwa kumpata Raheli. Ikawa machoni pake kama siku chache tu kwa vile alivyompenda. Yakobo akamwambia Labani, Nipe mke wangu, maana siku zangu zimetimia; niingie kwake. Labani akakusanya watu wote wa mahali pale, akafanya karamu. Ikawa wakati wa jioni akamtwaa Lea, binti yake, akamletea Yakobo, naye akaingia kwake. Labani akampa Lea mjakazi wake Zilpa, awe mjakazi wake. Ikawa, kulipokuwa asubuhi, kumbe! Ni Lea. Akamwambia Labani, Nini hii uliyonitenda? Sikukutumikia kwa Raheli? Mbona umenidanganya? Labani akasema, Havitendeki hivi kwetu, kumtoa mdogo kabla ya mkubwa;”



Utangulizi:

Hakuna linalotokea kwa bahati mbaya Duniani, wakati mwingine Mungu anaweza kuruhusu, ufanye kazi, au biashara, au huduma au usomee fani ambayo kimsingi inaweza ikawa sio chaguo lako, na hali kadhalika unaweza kuwa katika mahusiano na mtu ambaye moyo wako unaweza usiwe umemridhia moja kwa moja isipokuwa ni kwa sababu ya mazingira fulani, katika maisha yangu nimekuwa karibu na wanafunzi na walimu na watu wa kada mbalimbali za kitaaluma, na nimesikia kwa masikio yangu wengine wakisema nilitaka kuchukua masomo ya Sayansi, lakini walimu walinishauri nichukue masomo ya Sanaa, nilitaka kuchukua masomo ya Sanaa lakini wazazi wangu walinishauri nichukue Sayansi, nilitaka kuwa daktari lakini serikali ilinipangia ualimu, nilitaka kuwa mwanasheria lakini nililazimika kuwa mwanahabari, nilikuwa na mipango yangu kadhaa lakini nimejikuta nimekuwa Mwalimu, Mungu katika hekima yake wakati mwingine anaweza kuruhusu ubebe mzigo ambao moyo wako hungependelea kuubeba kwa kusudi la kutimiza mpango wake usioweza kuuona kwa wakati huo au kwa macho yako na sio hivyo tu wakati mwingine Mungu anaruhusu hivyo kwaajili ya ukuaji wa kiroho, kukufundisha kuacha mapenzi yako na kusikiliza ya kwake, kukufundisha uvumilivu, kupenda kisichoweza kupendeka na kukunyima kutimiza mapenzi yako uli uweze kujisalimisha kwenye mapenzi yake, hali kama hiyo ndiyo iliyomtokea Yakobo wakati anataka kuoa, alijiandaa na kufanya kazi kwa bidii kwaajili ya Raheli lakini akaozwa Lea bila kutaka!, Kumbe ni Lea badala ya Raheli.

Mwanzo 29:16-20 “Labani alikuwa na binti wawili, jina la mkubwa ni Lea, na jina la mdogo ni Raheli. Naye Lea macho yake yalikuwa dhaifu, lakini Raheli alikuwa mzuri wa umbo, na mzuri uso. Yakobo akampenda Raheli akasema, Nitakutumikia miaka saba kwa kumpata Raheli, binti yako mdogo. Labani akasema, Afadhali nikupe wewe kuliko mtu mwingine; kaa kwangu. Yakobo akatumika miaka saba kwa kumpata Raheli. Ikawa machoni pake kama siku chache tu kwa vile alivyompenda.”

Kuna maumivu kiasi fulani ambayo wengine wanaweza wasiyaseme kwa maneno lakini yakaishia moyoni, maumivu ya kupata ua kufanya jambo ambalo kimsingi hujalipenda toka moyoni, hujalitamani, hujalitaka wala hujaliomba, au hujalisomea, unaweza kabisa katika maisha ukasomea ujuzi fulani kisha ukapangiwa mwingine, unaweza kuomba kazi fulani na ukapewa nyingine unaweza kutarajia kuwa ungeoa mke wa aina fulani au ukaolewa na mume wa aina fulani, lakini ukaishia kuolewa na mwingine, ungetaka idadi fulani ya watoto au watoto wa jinsia fulan unashangaa umepewa wa aina fulanii, au ulikuwa na ndoto ya maisha fulani na ukajikuta unaishi maisha tofauti, haya ndiyo yaliyo mtokea Yakobo, alipoenda kwa mjomba wake kuoa alikuwa na nia ya kumpata Raheli na kimsingi alimpenda Raheli aliwekeza nguvu zake na akili zake na hisia zake kwa Raheli, na akatumika miaka saba ili ampate kipenzi wake Raheli lakini siku ya harusi yake anaamka asubuhi kumbe ni Lea! Hali hii inawakuta watu wengi,  katika maisha kujikuta kuwa wana kile walichokua hawajakitaka, ujumbe huu ni kwa watu wanaopitia hali kama hiyo na Mungu ana makusudi na wewe na anataka kusema nawe, tutajifunza ujumbe huu KUMBE NI LEA BADALA YA RAHELI kwa kuzingatia vipengele muhimu vitatu  vifuatavyo:-

·         Inapokuwa Lea badala ya Raheli

·         Kumbe ni Lea badala ya Raheli

·         Kusudi la Mungu kupitia Lea

Inapokuwa Lea badala ya Raheli

Wote tutakuwa tunakumbuka kuwa baada ya Yakobo kuchukua mbaraka wa Esau na mgogoro kujitokeza katika familia Rebeka alimshauri Isaka kuwa kijana wao na aende kwa kaka yake Rebeka yaani Labani ili ajipatie mke huko badala ya kujitwalia mke katikati ya Wakanaani ambao roho yake Rebeka haikuwaridhia, Yakobo alisafiri kuelekea Haran kwa mjomba wake Labani ili ajipatie mke huko na alipofika huko kimsingi Yakobo alimpenda sana Raheli kwa sababu ndiye aliyekuwa anamvutia kimwili na kiumbo na kwa uzuri, walipatana na mjomba wake kuwa mahari itakuwa ni kumtumikia kwa miaka 7 kwaajili ya Raheli, kwa hiyo Yakobo alifanya kazi kwa bidii sana kwaajili ya kile alichokuwa amekiona, amekitamani na kukipenda, mke wa ndoto yake, stori nzima iko hapa:-

Mwanzo 29:16-30 “Labani alikuwa na binti wawili, jina la mkubwa ni Lea, na jina la mdogo ni Raheli. Naye Lea macho yake yalikuwa dhaifu, lakini Raheli alikuwa mzuri wa umbo, na mzuri uso. Yakobo akampenda Raheli akasema, Nitakutumikia miaka saba kwa kumpata Raheli, binti yako mdogo. Labani akasema, Afadhali nikupe wewe kuliko mtu mwingine; kaa kwangu.Yakobo akatumika miaka saba kwa kumpata Raheli. Ikawa machoni pake kama siku chache tu kwa vile alivyompenda. Yakobo akamwambia Labani, Nipe mke wangu, maana siku zangu zimetimia; niingie kwake. Labani akakusanya watu wote wa mahali pale, akafanya karamu.Ikawa wakati wa jioni akamtwaa Lea, binti yake, akamletea Yakobo, naye akaingia kwake. Labani akampa Lea mjakazi wake Zilpa, awe mjakazi wake. Ikawa, kulipokuwa asubuhi, kumbe! Ni Lea. Akamwambia Labani, Nini hii uliyonitenda? Sikukutumikia kwa Raheli? Mbona umenidanganya? Labani akasema, Havitendeki hivi kwetu, kumtoa mdogo kabla ya mkubwa; timiza siku zake saba, nasi tutakupa huyu naye kwa utumishi utakaonitumikia, miaka saba mingine. Yakobo akafanya hivi, akatimiza siku zake saba. Naye akampa Raheli binti yake kuwa mkewe. Labani akampa binti yake Raheli mjakazi wake Bilha, awe mjakazi wake. Akaingia kwa Raheli naye, akampenda Raheli kuliko Lea, akatumika kwa ajili yake miaka saba mingine.”

Unaweza kuona mtu anafanya kazi kwa bidii na kwa kujituma kweli kweli akiwa na ndoto ya kumpata Raheli lakini hatimaye anakuja kupewa Lea, hili linaweza kuwa jambo lenye kuumiza sana kwamba unafanya kazi, unasoma au unajituma kwaajili ya malengo fulani alafu unakuja kujikuta ni kama ulimwengu unataka ufanye jambo lingine, jambo hili linaumiza, unatoa juhudi zako zote, unatoa muda wako wote, unawekeza moyo wako wote lakini matokeo yanakuwa sio yale uliyoyatarajia, hali hii iko hivyo duniani, kuna watu wamewapenda sana wachumba zao, wakawafulia, wakawapikia, wakawa wakiwajulia hali lakini na kuwapa kila kitu, lakini yule bwana akaja akaoa mwanamke mwingine, kuna watu wamejitoa kwaajili ya wachumba wao wakawasomesha wakawahudumia na kuwafadhili, hata wakafunga na kuomba kwaajili yao kwa kulia, lakini wakaja kuolewa na mwanaume mwingine, kuna watu walikuwa na ndoto ya kuendesha ndege lakini leo ni Askari polisi, kuna watu walitaka kuwa madaktari lakini leo ni walimu, Moyo wako unaweza kuchoka na kuumia na kuumizwa na matarajio yaliyovunjika na unaweza kujiuliza Mungu kwa nini hali hii inakuwa hivi? Unasomea fani Fulani kisha unakuja kupata kazi flani tofauti na ile uliyoisomea na iliyoko moyoni mwako! Wala sicho ulichokitarajia, unahisi kuchanganyikiwa, unahisi kuumia na unaanza kumuhoji Mungu! Imekuwaje? Ndoto yangu ilikuwa hii mbona nafanya jambo hili?

Mithali 13:12 “Kilichotarajiwa kikikawia kuja, moyo huugua. Bali haja ya mtu ikipatikana, ni mti wa uzima.”

Tunao watu wengi sana leo hii katika jamii ambao mioyo yao imejeruhiwa kwa kuwa na matokeo wasiyoyatarajia, mtu amesoma kwa bidii na kufanya mtihani wake kwa umakini anakuja kupata Division three ambayo hakuitegemea, unaweza kuolewa na mume ambaye  hata hukuwa na hata hisia naye, unaweza kuwa na mke ambaye huna hata hisia naye lakini mnajikuta ndio mnaishi, yako maisha ambayo unaweza kuwa ndani yake lakini moyo wako ukawa haupo humo, haki hii ndiyo ilityomtokea Yakobo anampenda Raheli na ameganya kqzi miaka saba kwaajili yake, lakini amepewa Lea, kwa hiyo katika maisha yetu inapokuwa Lea badala ya Raheli watu hukosa amani na furaha na kuona kama maisha yameshakataa na wakati mwingine unaweza kuwaza na kufikiri umekosea wapi katika kaninu za maisha, unaweza kujikuta hufurahii maisha, hufurahii kazi, unakosa furaha kwa kile ulichonacho na ukijilinganisha na wengine ndio unachoka unaweza kudhani wewe una balaa, lakini nataka nikugusie kuwa Mungu ana mpango!, Hakuna jambo lolote linalotokeaau kukupata nje ya mpango wa Mungu, hapa duniani hatujaja kutimiza mpango wetu, tumekuja duniani kutimiza mpango na mapenzi ya Mungu, hivyo sio jambo la ajabu yakakupata yaliyo mageni

Kumbe ni Lea badala ya Raheli

Neno la Mungu linaonyesha ya kuwa njia za Mungu ziko juu sana kuliko njia za mwanadamu na wala mawazo yetu si kama mawazo yake, njia za Mungu ziko juu sana, mpango wa Mungu ni mkuu kuliko matakwa ya mwanadamu, Mungu hafanyi kazi kwa kusikiliza hisia zeu, ana mpango mkubwa sana kuliko hisia zako, Hapa duniani ulizaliwa kwa kusudi la Mungu na kwa sababu hiyo mwenye mji wake ni Mungu na mwenye mpango wake ni yeye kwa hiyo wewe unaweza kumtaka Raheli lakini Mungu akakupa Lea, unaweza kudhani kuwa dunia imekulazimisha Lea na we ulitaka Raheli lakini, Lea ndio mpango kamili wa Mungu. Raheli unaweza kuwa sio mpango wa kudumu wala wa milele lakini Lea unaweza kuwa mpango wa Mungu wa kudumu na wa milele, na wenye faida unajua nini  watoto wote maalumu ambao Mungu alikuwa na kusudi lake la kudumu walipita kwa Lea na sio Raheli

Mwanzo 29:31-35 “BWANA akaona ya kwamba Lea hakupendwa, naye akafungua tumbo lake; bali Raheli alikuwa hazai. Lea akapata mimba akazaa mwana, akampa jina lake, Reubeni, maana alisema, Kwa kuwa BWANA ameona teso langu; sasa mume wangu atanipenda. Akapata mimba tena akazaa mwana, akasema, Kwa kuwa BWANA amesikia ya kwamba mimi sikupendwa, amenipa na huyu; akamwita jina lake Simeoni. Akapata mimba tena, akazaa mwana, akasema, Basi wakati huu mume wangu ataungana nami, kwa sababu nimemzalia wana watatu. Kwa hiyo akamwita jina lake Lawi. Akapata mimba tena, akazaa mwana. Akasema, Mara hii nitamsifu BWANA; kwa hiyo akamwita jina lake Yuda; akaacha kuzaa.”

Mungu aliwatumia Walawi, kutoka kwa Lea kuwa makuhani kwaajili ya utumishi wa Mungu katika nyumba yake na Mungu na Mungu alimtumia Yuda kutoka kwa Lea kuleta viongozi mashuhuri na wacha Mungu kama Daudi na kupitia Lea na Yuda alimleta Yesu Kristo

Mathayo 1:1-2.“Kitabu cha ukoo wa Yesu Kristo, mwana wa Daudi, mwana wa Ibrahimu. Ibrahimu alimzaa Isaka; Isaka akamzaa Yakobo; Yakobo akamzaa Yuda na ndugu zake;”

Mungu aliruhusu Lea kuwepo katika maisha ya Yakobo kwa sababu Lea ndio ulikuwa mpango wa Mungu, Lea alikuwa ni darasa la unyenyekevu, Lea alikuwa ni chuo cha uvumilivu, Lea alikuwa ni shule ya haki ya Mungu, Lea ilikuwa ni shule ya kujifunza kupenda kile ambacho Mungu amekupangia, Mungu anatufundisha kumfuata yeye na sio hisia zetu, Lazima ufike wakati katika maisha yetu tuamue kufuata hisia zetu au kutimiza mpango wa Mungu, Lea alilazimika kutaka kumpendeza Yakobo lakini hata pamoja na kumzalia watoto wengi wa kume mfuluzizo bado Yakobo hakuona nguvu za Mungu, Lea aliamua kumuita mtoto wake Yuda akisema NITAMSIFU BWANA Furaha ya kweli haipatikani kwa wanadamu bali inapatikana kwa Mungu, Mungu aliona kitu ndani ya Lea ambacho kimsingi hakikuweko ndani ya Raheli Mungu anaona kile ambacho wanadamu hawakioni, Lea hakuwa mzuri wa uso lakini alikuwa mzuri moyoni, Yule aliyeyependwa na aliyekuwa mzuri wa uso moyoni hakuwa ameshikamana na Mungu na aliibeba  kwa kuiiba miungu ya baba yake na alikufa baaadae kwa neno la Yakobo ona:-

Mwanzo 31:19-35 “Basi Labani alikuwa amekwenda kuwakata manyoya kondoo zake, na Raheli akaviiba vinyago vya babaye. Yakobo akamhadaa Labani, Mshami, kwa kuwa hakumwambia ya kwamba anakimbia. Basi akakimbia yeye na yote aliyokuwa nayo; akaondoka akauvuka mto, akaelekeza uso wake kwenda mlima wa Gileadi. Hata siku ya tatu Labani akaambiwa ya kwamba Yakobo amekimbia, akatwaa ndugu zake pamoja naye, akamfuata mwendo wa siku saba. Akampata katika mlima wa Gileadi. Mungu akamjia Labani, Mshami, katika ndoto ya usiku, akamwambia, Ujihadhari, usimwambie Yakobo neno la heri wala la shari. Labani akamfikia Yakobo, na Yakobo alikuwa amepiga hema zake katika mlima, na Labani na ndugu zake wakapiga hema zao katika mlima wa Gileadi. Labani akamwambia Yakobo, Umefanya nini? Umenihadaa, ukawachukua binti zangu kama mateka waliotwaliwa kwa upanga. Mbona umekimbia kwa siri ukanihadaa, wala hukuniambia, nipate kuagana nawe uende zako kwa furaha, na nyimbo, na ngoma, na kinubi? Wala hukuniacha niwabusu wanangu, na binti zangu; basi umetenda upumbavu. Ninao uwezo mkononi mwangu wa kukufanyia madhara; lakini Mungu wa baba yako usiku huu ameniambia, akisema, Ujihadhari, usimwambie Yakobo neno la heri wala la shari. Basi sasa, umetoka kwa sababu umetamani sana nyumba ya baba yako. Mbona basi umeiiba miungu yangu? Yakobo akajibu, akamwambia Labani, Kwa sababu naliogopa, nikasema, Usije ukaninyang'anya binti zako kwa nguvu. Awaye yote utakayemwona kuwa nayo miungu yako, yeye asiishi. Mbele ya ndugu zetu ukitambue kilicho chako kwangu, ukakichukue. Maana Yakobo hakujua ya kwamba Raheli ameiiba. Labani akaingia katika hema ya Yakobo, na hema ya Lea, na hema ya vijakazi wawili, wala hakuiona. Akatoka katika hema ya Lea, akaingia katika hema ya Raheli. Basi Raheli alikuwa amevitwaa vile vinyago ameviweka katika matandiko ya ngamia, na kuvikalia. Labani akapapasa hema yote wala hakuviona. Naye Raheli akamwambia babaye, Bwana wangu asikasirike kwa sababu siwezi kuinuka mbele yako, maana nimeshikwa na mambo ya kike. Akatafuta, wala hakuviona vile vinyago.”

Raheli alikuwa muabudu miungu, aliiba miungu ya baba yake Neno vinyago linalotajwa hapo katika Kiebrania linatajwa kama “Teraphim” ambao ni miungu midogo midogo yenye sura kama ya mwanadamu ambayo ilichongwa na kuabudiwa zamani hasa huko mashariki ya mbali na ambayo ilitumika kwa uganga na uchawi na kupigia ramli, miungu hii ilichongwa kwa mfano wa wanadamu na iliyorithiwa toka mababu na mababu na ilirithishwa kwa viongozi wa familia kwa hiyo kuwa na miungu hiyo kulimaanisha kutaka kuwa kiongozi wa familia  na Labani alipokuja kuulizia miungu hiyo Raheli aliificha, Yakobo bila kuelewa alimwambia  Labani yeye atakayekutwa na miungu yako na asiishi, tukio hili lilipelekea kifo cha mapema cha Raheli, Kumbe Lea alimuabudu Mungu wa kweli lakini Raheli miungu!

Mwanzo 35:16-18 “Wakasafiri kutoka Betheli, hata ukabaki mwendo wa kitambo tu kufika Efrathi, Raheli akashikwa na utungu wa kuzaa, na utungu wake ulikuwa mzito. Ikawa alipokuwa anashikwa sana na utungu, mzalisha akamwambia, Usiogope, maana sasa utamzaa mwanamume mwingine. Ikawa hapo katika kutoa roho yake, maana alikufa, akamwita jina lake Benoni, lakini babaye alimwita Benyamini.”

Je bado una huzuni ya kumkosa Raheli? Mungu alikuwa na mpango, sio kila Raheli ni Baraka na sio kila Lea ni Laana wakati mwingine Raheli ni tamaa yako na Lea ni mapenzi ya Mungu kwako, Mpango wa Mungu haujafichwa ndani ya kile unachikipenda bali uko ndani ya kile alichokupa, acha kutokukubaliana na Lea katika maisha yako, Lea sasa anahitaji upendo wako, ni muhimu sasa ukakubaliana na kile ambacho Mungu amekiruhusu katika maisha yako, ni lazima ukubali mapenzi ya Mungu na kutafuta kusudi la ndani la hali uliyo nayo, badala ya kujutia kile ulichonyimwa furahia kile ulichopewa na Mungu na kipokee kwa shukurani maana katika hilo uko mpango wa Mungu, Yesu anatoka kwa Lea na sio kwa Raheli, kile usichokipenda kinaweza kubeba hatima yako! Na kusudi la Mungu katika mpango wake, yako mambo tunaweza kuchagua na yako mambo Mungu mwenyewe anakuchagulia, furahia kile Mungu amekuchagulia, hakuna bahati mbaya katika kile Mungu amekupangia, oooo kumbe ni Lea badala ya Raheli.

Kusudi la Mungu kupitia Lea

Mungu anataka kutufunza hapa kuwa wakati mwingine katika hekima yake atafanya mambo kinyume na yale tunayoyatarajia ambayo kimsingi ni shauku na tamaa zetu au hisia zetu, Mungu anataka kuivunja ile hali ya kujitegemea katika maamuzi yetu anataka ukomavu anataka kurekebisha tabia zetu anataka kutuumbia moyo wa kuwa na uhusiano wa karibu sana na yeye ili tumtegemee yeye, hali hizo zote zinaruhusiwa kwaajili ya ukamilifu wetu kwa hiyo wale wote ambao wako katika hali kama ile aliyoipitia Yakobo wanapaswa kuelewa kuwa ni mchakao wa Mungu utimize mapenzi yake na sio ya kwako kwa hiyo fanya kwa upendo na uaminifu kile ambacho Mungu amekuchagulia.

Warumi 8:28-29 “Nasi twajua ya kuwa katika mambo yote Mungu hufanya kazi pamoja na wale wampendao katika kuwapatia mema, yaani, wale walioitwa kwa kusudi lake. Maana wale aliowajua tangu asili, aliwachagua tangu asili wafananishwe na mfano wa Mwana wake, ili yeye awe mzaliwa wa kwanza miongoni mwa ndugu wengi.”

Mungu anataka tuache kujitegemea na kujitumainia na badala yake tuishi kwa kumtegemea yeye, Mungu ataupiga chini mpango wetu wa ubinafsi na atabadilisha mambo ili tumtegemee yeye

2Wakorintho 12:7-9. “Na makusudi nisipate kujivuna kupita kiasi, kwa wingi wa mafunuo hayo nalipewa mwiba katika mwili, mjumbe wa Shetani ili anipige, nisije nikajivuna kupita kiasi. Kwa ajili ya kitu hicho nalimsihi Bwana mara tatu kwamba kinitoke.Naye akaniambia, Neema yangu yakutosha; maana uweza wangu hutimilika katika udhaifu. Basi nitajisifia udhaifu wangu kwa furaha nyingi, ili uweza wa Kristo ukae juu yangu.”

Mungu anataka utii hata katika mazingira magumu, kwa msingi huo badala ya kujiuliza kwanini mimi ninayapitia haya wewe jiulize Mungu atatukuzwaje kwenye jambo hili, Je kwa kuwa tumepewa uhuru wa kuchagua wadhani ya kuwa Mungu hana nafasi ya kuonyesha ubwana wake katika maisha yetu? Ubinafsi wetu na starehe zetu lazima zife linapokuja swala la kutimiza mpango wa Mungu, Kumbe ni Lea badala ya Raheli.

Na. Rev. Innocent Samuel Kamote

Mkuu wa wajenzi mwenye Hekima

Jumapili, 14 Juni 2026

Huyu ndiye Mwanangu, mpendwa, msikieni yeye!


Mathayo 17:1-5 “Na baada ya siku sita Yesu akawatwaa Petro, na Yakobo, na Yohana nduguye, akawaleta juu ya mlima mrefu faraghani; akageuka sura yake mbele yao; uso wake ukang'aa kama jua, mavazi yake yakawa meupe kama nuru. Na tazama, wakatokewa na Musa na Eliya, wakizungumza naye. Petro akajibu akamwambia Yesu, Bwana, ni vizuri sisi kuwapo hapa; ukitaka, nitafanya hapa vibanda vitatu, kimoja chako wewe, na kimoja cha Musa, na kimoja cha Eliya. Alipokuwa katika kusema, tazama, wingu jeupe likawatia uvuli; na tazama, sauti ikatoka katika lile wingu, ikasema, Huyu ni Mwanangu, mpendwa wangu, ninayependezwa naye; msikieni yeye.”


 

Utangulizi.

Moja ya maneno ya msingi ambayo dunia inapaswa kuyazingatia ni haya yaliyowahi kutamkwa na Mungu Baba mwenyewe katika mlima wa ugeuko (transfiguration) mbele ya Petro Yakobo na Yohana. Kauli hii ni moja ya kauli nzito sana katika Agano jipya kwa sababu ni kauli yenye mamlaka kubwa nayomtambulisha Bwana wetu Yesu Kristo kwa mamlaka kubwa ili kwamba wanadamu wote wamsikilize kumtii na kumfuata Kauli hii imerejewa kwa msisitizo katika njili zile tatu zifananazo, Mathayo, Marko na Luka.

Marko 9:2-7 “Hata baada ya siku sita Yesu akawatwaa Petro, na Yakobo, na Yohana, akawaleta juu ya mlima mrefu faraghani, peke yao; akageuka sura yake mbele yao; mavazi yake yakimeta-meta, meupe mno, jinsi asivyoweza dobi duniani kuyafanya meupe. Wakatokewa na Eliya pamoja na Musa, nao walikuwa wakizungumza na Yesu.Petro akajibu, akamwambia Yesu, Rabi, ni vizuri sisi kuwapo hapa; na tufanye vibanda vitatu, kimoja chako wewe, kimoja cha Musa, na kimoja cha Eliya. Maana, hakujua la kunena, kwa kuwa waliingiwa na hofu nyingi. Kisha likatokea wingu, likawatia uvuli; sauti ikatoka katika lile wingu, Huyu ni Mwanangu, mpendwa wangu, msikieni yeye.”

Luka 9:28-35 “Baada ya maneno hayo yapata siku nane, aliwatwaa Petro na Yohana na Yakobo, akapanda mlimani ili kuomba. Ikawa katika kusali kwake sura ya uso wake ikageuka, mavazi yake yakawa meupe, yakimeta-meta. Na tazama, watu wawili walikuwa wakizungumza naye, nao ni Musa na Eliya; walioonekana katika utukufu, wakanena habari za kufariki kwake atakakotimiza Yerusalemu.Petro na wale waliokuwa pamoja naye walikuwa wamelemewa na usingizi; lakini walipokwisha amka waliuona utukufu wake, na wale wawili waliosimama pamoja naye. Ikawa hao walipokuwa wakijitenga naye, Petro alimwambia Yesu, Bwana mkubwa, ni vizuri sisi kuwapo hapa; na tufanye vibanda vitatu; kimoja chako wewe, na kimoja cha Musa, na kimoja cha Eliya; hali hajui asemalo. Alipokuwa akisema hayo, lilitokea wingu likawatia uvuli, wakaogopa walipoingia katika wingu hilo. Sauti ikatoka katika wingu, ikisema, Huyu ni Mwanangu, mteule wangu, msikieni yeye.”

Injili zote tatu zifananazo (Synoptic Gospel) zimerekodi tukio hili muhimu, lililoshuhudiwa na Petro, Yakobo na Yohana kwa sababu ya umuhimu wake mkubwa ambao leo tutachukua muda kuutafakari na kuusisitiza kwa jamii ili kila mtu duniani apate kusadiki ya kuwa Yesu ni mwana wa Mungu na kwamba yeye ndiye njia na kweli na uzima na hakuna mwingine kabla yake na baada yake, umuhimu wa tukio hili kwa mtazamo wangu hauko katika kubadilika sura kwa Yesu Kristo, wala katika kutokewa na Musa na Eliya lakini uzito mkubwa wa tukio hili uko katika sauti ile “Huyu ndiye Mwanangu, mpendwa, msikieni yeye!”, tutajifunza somo hili HUYU NDIYE MWANANGU MPENDWA MSIKIENI YEYE kwa kuzingatia vipengele muhimu vitatu vifuatavyo:-

·         Maana ya neno Msikieni yeye!

·         Umuhimu wa Yesu Kristo kwa wanadamu.

·         Huyu ndiye Mwanangu mpendwa msikieni yeye.

Maana ya neno Msikieni yeye

Wote tutakuwa tunafahamu kuwa neno la Kiebrania kuhusu kusikia linajulikana kama neno “SHEMA” maana yake katika kiingereza “hear” or “Listen” “understand” “Obey” or “take action”neno hili lina uzito mkubwa sana katika maandiko ya Kiebrania sio kwaajili ya kusikia sauti pekee bali kusikia, kutii na kutekeleza, neno hilo likifanyiwa kazi kimsingi lina Baraka kubwa sana na lisipofanyiwa kazi linasababisha laana mikosi na balaa, kwa hiyo kila Myahudi alisisitizwa kuwa na bidii katika kusikia, utaisikiliza sauti ya Bwana Mungu wako, huu ulikuwa ni msisitizo wa kitorati

Kumbukumbu 6:3-5 “SIKIZA BASI, EE ISRAELI, ukaangalie kuzitenda; upate kufanikiwa, mpate kuongezeka sana, kama Bwana, Mungu wa baba zako, alivyokuahidi, katika nchi ijaayo maziwa na asali. Sikiza, Ee Israeli; Bwana, Mungu wetu, Bwana ndiye mmoja. Nawe mpende Bwana, Mungu wako, kwa moyo wako wote, na kwa roho yako yote, na kwa nguvu zako zote.”

Kutoka 19:5-6 “Sasa basi IKIWA MTAITII SAUTI YANGU kweli kweli, na kulishika agano langu, hapo ndipo mtakapokuwa tunu kwangu kuliko makabila yote ya watu; maana dunia yote pia ni mali yangu, nanyi mtakuwa kwangu ufalme wa makuhani, na taifa takatifu. Hayo ndiyo maneno utakayowaambia wana wa Israeli.”

Kumbukumbu 28:1-2 “Itakuwa UTAKAPOSIKIA SAUTI YA BWANA, Mungu wako, kwa bidii, kutunza kuyafanya maagizo yake yote nikuagizayo leo, ndipo Bwana, Mungu wako, atakapokutukuza juu ya mataifa yote ya duniani;na baraka hizi zote zitakujilia na kukupata usikiapo sauti ya Bwana, Mungu wako.”

Kutoka 23:20-26 “Tazama, mimi namtuma malaika aende mbele yako, ili akulinde njiani na kukupeleka mpaka mahali pale nilipokutengezea. Jitunzeni mbele yake, mwisikize sauti yake; wala msimtie kasirani; maana, hatawasamehe makosa yenu; kwa kuwa jina langu limo ndani yake. Lakini UKIISIKIZA SAUTI yake kweli, na KUYATENDA YOTE ninenayo mimi; ndipo mimi nitakuwa ni adui wa adui zako, na mtesi wa hao wakutesao. Kwa kuwa malaika wangu atatangulia mbele yako, na kukufikisha kwenye Mwamori, na Mhiti, na Mperizi, na Mkanaani, na Mhivi, na Myebusi; nami nitawakatilia mbali. Usiisujudie miungu yao, wala kuitumikia; wala usitende mfano wa matendo yao; bali utaiangamiza kabisa, na nguzo zao utazivunja vipande vipande. Nanyi mtamtumikia BWANA, Mungu wenu, naye atakibarikia chakula chako, na maji yako; nami nitakuondolea ugonjwa kati yako. Hapatakuwa na mwenye kuharibu mimba, wala aliye tasa, katika nchi yako; na hesabu ya siku zako nitaitimiza.”

Kwa hiyo kama wanafunzi wa Biblia utakuwa umegundua kuwa neno kusikia, sikia, msikilizeni, tiini, linaambatana na baraka kubwa sana ulimwenguni, endapo watu wa Mungu watajifunza na kuelewa kuwa kusikia, kuna maana ya kutii, kutunza, kufanya, kuishi, kuamini na kufuata na ndani ya neno hili kuna siri kubwa sana ya Baraka za Mungu ni kama Baraka zote zimefungwa katika kusikiliza kunakotajwa kimaandiko yaani SHEMA basi kumsikia Yesu ni Baraka.

Kwa hiyo Sauti ya Mungu Baba iliposikika kwa Petro, Yakobo na Yohana Huyu ndiye mwanangu mpendwa msikieni yeye, wanafunzi hawa wa Yesu Kristo kwa kuwa walikuwa Wayahudi walikuwa na uelewa mpana wa kile ambacho mbingu zilikuwa zinakimaanisha kuhusu Yesu Kristo, mwanaye ni kwamba uko ulazima au amri kuwa yeye ni wa kuaminiwa, yeye ndiye wa kumtii, yeye ndiye wa kumfuata, yeye ndiye wa kumtegemea, yeye ndiye wa kusikilizwa, yeye ndiye wa kufuata maagizo yake yeye ndiye wa kutekeleza asemayo na hakuna mwingine kabla yake wala baada yake, Ni lazima wafuate mafundisho yake na kwa kumtii yeye Baraka zote zilizoahidiwa katika maandiko zitatufuata

Umuhimu wa Yesu Kristo kwa wanadamu.

Mathayo 17:1-5 “Na baada ya siku sita Yesu akawatwaa Petro, na Yakobo, na Yohana nduguye, akawaleta juu ya mlima mrefu faraghani; akageuka sura yake mbele yao; uso wake ukang'aa kama jua, mavazi yake yakawa meupe kama nuru. Na tazama, wakatokewa na Musa na Eliya, wakizungumza naye. Petro akajibu akamwambia Yesu, Bwana, ni vizuri sisi kuwapo hapa; ukitaka, nitafanya hapa vibanda vitatu, kimoja chako wewe, na kimoja cha Musa, na kimoja cha Eliya. Alipokuwa katika kusema, tazama, wingu jeupe likawatia uvuli; na tazama, sauti ikatoka katika lile wingu, ikasema, Huyu ni Mwanangu, mpendwa wangu, ninayependezwa naye; MSIKIENI yeye.”

Tukio hili katika maandiko ni tukio la kipekee lisiloweza kusahaulika, Petro katika maisha yake yote aliweza kumtumikia Mungu kwa jina la Yesu na hata miaka mingi sana ilipopita bado aliendelea kulikumbuka tukio hili lililokuwa limemfunua Yesu Kristo katika ubora wake na kama Bwana aliyekubalika kwa mamlaka kubwa zaidi kuliko yeyote yule, hata wale walioheshimika sana  katika jamii ya Israel kama Musa na Eliya akam manabii wakubwa na muhimu sana, Petro hata alipokuwa anakaribia kufa bado alikumbuka tukio lile la kipekee, la kufunuliwa kwa heshima na utukufu na kuthibitishiwa ukuu wa Yesu Kristo kuliko manabii wote, kulikofanywa na Mungu Baba:-

2Petro 1:16-18 “Maana hatukufuata hadithi zilizotungwa kwa werevu, tulipowajulisha ninyi nguvu zake Bwana wetu Yesu Kristo na kuja kwake; bali tulikuwa tumeuona wenyewe ukuu wake. Maana alipata kwa Mungu Baba heshima na utukufu, hapo alipoletewa sauti iliyotoka katika utukufu mkuu, Huyu ni Mwanangu, mpendwa wangu, ninayependezwa naye. NA SAUTI HIYO SISI TULIISIKIA ikitoka mbinguni tulipokuwa pamoja naye katika mlima ule mtakatifu”.

Mungu alitaka Petro, Yakobo na Yohana na walimwengu wote baada yao, kuwa na uelewa huu mkubwa kuhusu Yesu Kristo ili asitokee mtu akamvunjia Yesu Heshima, Yesu ni mkuu na mbora kuliko nabii Musa, Eliya na wengine wote, sio tu kuwa torati na manabii zilizungumza habari zake lakini hata Mungu Baba mwenyewe alithibitisha habari zake na kina Petro waliisikia sauti, iliyowathibitishia kuwa sifa za Yesu sio hadithi za kutungwa kwa werevu bali ni uthibitisho kutoka mbinguni kuwa Yesu ni mwana wa Mungu na ulimwengu unapaswa kumuamini yeye na kumtii;-

-          Maandiko yote yanaelekeza kwa Yesu Kristo – Unapoyachambua maandiko yote kutoka agano la kale mpaka mwisho kuanzia Torati na manabii wote walielekeza watu kwa Yesu Kristo na ukiona nabii anaelekeza watu kwa mtu mwingine na sio Kristo huyo ni nabii wa uongo, au ukiona nabii anaelekeza watu wamwamini yeye na sio Yesu Kristo basi huyo ni nabii wa uongo, Yesu Kristo ndio ufunuo wa mwisho wa Mungu kwa wanadamu wote.

Luka 24:25-31 “Akawaambia, Enyi msiofahamu, wenye mioyo mizito ya kuamini yote waliyoyasema manabii! Je! Haikumpasa Kristo kupata mateso haya na kuingia katika utukufu wake? Akaanza kutoka Musa na manabii wote, akawaeleza katika maandiko yote mambo yaliyomhusu yeye mwenyewe. Wakakikaribia kile kijiji walichokuwa wakienda, naye alifanya kama anataka kuendelea mbele.Wakamshawishi wakisema, Kaa pamoja nasi, kwa kuwa kumekuchwa, na mchana unakwisha. Akaingia ndani kukaa nao. Ikawa alipokuwa ameketi nao chakulani, alitwaa mkate, akaubariki, akaumega, akawapa. Yakafumbuliwa macho yao, wakamtambua; kisha akatoweka mbele yao.”

-          Musa ingawa alikuwa nabii mkubwa lakini aliwaelekeza watu kwa Yesu – Na kuamuru watu wote wamsikilize yeye yaani wamwamini, wamtii na kuyashika mafundisho yake, mtu awaye yote ambaye hatamsikiliza atakufa

Kumbukumbu 18:15-18 “Bwana, Mungu wako, atakuondokeshea nabii miongoni mwa ndugu zako kama nilivyo mimi; MSIKILIZENI YEYE. Kama vile ulivyotaka kwa Bwana, Mungu wako, huko Horebu, siku ya kusanyiko, ukisema, Nisisikie tena sauti ya Bwana, Mungu wangu, wala nisiuone tena moto huu mkubwa, nisije nikafa. Bwana akaniambia, Wametenda vema kusema walivyosema. Mimi nitawaondokeshea nabii miongoni mwa ndugu zao mfano wako wewe, nami nitatia maneno yangu kinywani mwake, naye atawaambia yote nitakayomwamuru.”

Matendo 3:22-24 “Kwa maana Musa kweli alisema ya kwamba, Bwana Mungu wenu atawainulieni nabii, katika ndugu zenu, kama MIMI; MSIKIENI YEYE katika mambo yote atakayonena nanyi. Na itakuwa ya kwamba kila mtu ASIYEMSIKILIZA NABII HUYO ATAANGAMIZWA na kutengwa na watu wake. Naam, na manabii wote tangu Samweli na wale waliokuja baada yake, wote walionena, walihubiri habari za siku hizi.”

-          Isaya alimuhubiri Kristo – Isaya alijulikana kama muhubiri mkubwa sana wa nyakati za agano la kale watu wengi wanamuita nabii wa Masihi au mwinjilishi wa agano la kale yeye alipewa neema ya kutoa unabii ulio wazi sana kuhusu Yesu Kristo ikiwepo mamlaka yake, kuzaliwa kwake na mateso yake akimuelezea Kristo miaka 700 kabla yake kwa uweza wa ajabu sana Isaya alimuhubiri Kristo na kumtaja kama mshauri wa ajabu, Mungu mwenye nguvu, baba wa milele na mfalme wa Amani, sasa utapata wapi uzima na uponyaji na wokovu kama humsikilizi?

Isaya 7:14 “Kwa hiyo Bwana mwenyewe atawapa ishara. Tazama, bikira atachukua mimba, atazaa mtoto mwanamume, naye atamwita jina lake Imanueli.”

Isaya 9:6 “Maana kwa ajili yetu mtoto amezaliwa, Tumepewa mtoto mwanamume; Na uweza wa kifalme utakuwa begani mwake; Naye ataitwa jina lake, Mshauri wa ajabu, Mungu mwenye nguvu, Baba wa milele, Mfalme wa amani.”

Isaya 53:1-9 “Ni nani aliyesadiki habari tuliyoileta? Na mkono wa Bwana amefunuliwa nani? Maana alikua mbele zake kama mche mwororo, Na kama mzizi katika nchi kavu; Yeye hana umbo wala uzuri; Na tumwonapo hana uzuri hata tumtamani. Alidharauliwa na kukataliwa na watu; Mtu wa huzuni nyingi, ajuaye sikitiko; Na kama mtu ambaye watu humficha nyuso zao, Alidharauliwa wala hatukumhesabu kuwa kitu.Hakika ameyachukua masikitiko yetu, Amejitwika huzuni zetu; Lakini tulimdhania ya kuwa amepigwa, Amepigwa na Mungu, na kuteswa. Bali alijeruhiwa kwa makosa yetu, Alichubuliwa kwa maovu yetu; Adhabu ya amani yetu ilikuwa juu yake, Na kwa kupigwa kwake sisi tumepona.Sisi sote kama kondoo tumepotea; Kila mmoja wetu amegeukia njia yake mwenyewe; Na Bwana ameweka juu yake Maovu yetu sisi sote.Alionewa, lakini alinyenyekea, Wala hakufunua kinywa chake; Kama mwana-kondoo apelekwaye machinjoni, Na kama vile kondoo anyamazavyo Mbele yao wakatao manyoya yake; Naam, hakufunua kinywa chake. Kwa kuonewa na kuhukumiwa aliondolewa; Na maisha yake ni nani atakayeisimulia? Maana amekatiliwa mbali na nchi ya walio hai; Alipigwa kwa sababu ya makosa ya watu wangu. Wakamfanyia kaburi pamoja na wabaya; Na pamoja na matajiri katika kufa kwake; Ingawa hakutenda jeuri, Wala hapakuwa na hila kinywani mwake.”

-          Yohana mbatizaji alimuhubiri Kristo na kuonyesha kuwa ni mwenye mamlaka kuu  – Yohana 1:26-30 “Yohana akawajibu akisema, Mimi nabatiza kwa maji. Katikati yenu amesimama yeye msiyemjua ninyi. Ndiye yule ajaye nyuma yangu, ambaye mimi sistahili kuilegeza gidamu ya kiatu chake. Hayo yalifanyika huko Bethania ng'ambo ya Yordani, alikokuwako Yohana akibatiza. Siku ya pili yake amwona Yesu anakuja kwake, akasema, TAZAMA, MWANA-KONDOO WA MUNGU, aichukuaye dhambi ya ulimwengu! Huyu ndiye niliyenena habari zake ya kwamba, Yuaja mtu nyuma yangu, ambaye amekuwa mbele yangu; kwa maana alikuwa kabla yangu.”

Yohana 3:26-31 “Wakamwendea Yohana, wakamwambia, Rabi, yeye aliyekuwa pamoja nawe ng'ambo ya Yordani, yeye uliyemshuhudia, tazama, huyo anabatiza na watu wote wanamwendea.Yohana akajibu, akasema, Hawezi mtu kupokea neno lo lote isipokuwa amepewa kutoka mbinguni. Ninyi wenyewe mwanishuhudia ya kwamba nalisema, Mimi siye Kristo, bali nimetumwa mbele yake. Aliye naye bibi arusi ndiye bwana arusi; lakini rafiki yake bwana arusi, yeye anayesimama na kumsikia, aifurahia sana sauti yake bwana arusi. Basi hii furaha yangu imetimia. Yeye hana budi kuzidi, bali mimi kupungua. Yeye ajaye kutoka juu, huyo yu juu ya yote. Yeye aliye wa dunia, asili yake ni ya dunia, naye anena mambo ya duniani. Yeye ajaye kutoka mbinguni yu juu ya yote.”           

-          Daudi – alihubiri na kutabiri kwa kina sana kwa habari ya mambo mengi kuhusu Yesu Kristo, na alimuita Bwana na kutabiri swala zima la kuketi katika mkono wa kuume wa Mungu huko mbinguni ona :-

 

Zaburi 110:1-2 “Neno la Bwana kwa Bwana wangu, Uketi mkono wangu wa kuume, Hata niwafanyapo adui zako Kuwa chini ya miguu yako. Bwana atainyosha toka Sayuni Fimbo ya nguvu zako. Uwe na enzi kati ya adui zako;”

Mathayo 22:41-46 “Na Mafarisayo walipokusanyika, Yesu aliwauliza, akisema, Mwaonaje katika habari za Kristo? Ni mwana wa nani? Wakamwambia, Ni wa Daudi. Akawauliza, Imekuwaje basi Daudi katika Roho kumwita Bwana, akisema, Bwana alimwambia Bwana wangu, Uketi mkono wangu wa kuume, Hata niwawekapo adui zako Kuwa chini ya miguu yako? Basi, Daudi akimwita Bwana, amekuwaje ni mwanawe? Wala hakuweza mtu kumjibu neno; wala hakuthubutu mtu ye yote tangu siku ile kumwuliza neno tena.”

-          Paulo mtume alimuelezea Yesu kwa kina sana - Wafilipi 2:5-11 “Iweni na nia iyo hiyo ndani yenu ambayo ilikuwamo pia ndani ya Kristo Yesu; ambaye yeye mwanzo alikuwa yuna namna ya Mungu, naye hakuona kule kuwa sawa na Mungu kuwa ni kitu cha kushikamana nacho; bali alijifanya kuwa hana utukufu, akatwaa namna ya mtumwa, akawa ana mfano wa wanadamu; tena, alipoonekana ana umbo kama mwanadamu, alijinyenyekeza akawa mtii hata mauti, naam, mauti ya msalaba. Kwa hiyo tena Mungu alimwadhimisha mno, akamkirimia Jina lile lipitalo kila jina; ili kwa jina la Yesu kila goti lipigwe, la vitu vya mbinguni, na vya duniani, na vya chini ya nchi; na kila ulimi ukiri ya kuwa YESU KRISTO NI BWANA, kwa utukufu wa Mungu Baba.”

Kila muhubiri nyakati za kanisa la kwanza alimuhubiri Kristo, kujulikana kwetu, kuheshimika kwetu hakutakuja kwa sababu ya kujijengea jina kutakuja kama tunamuinua Yesu Kristo katika maisha yetu na mahubiri yetu, kazi ya kila mtumishi wa Mungu ni kuwaelekeza watu wa Mungu kwa Yesu Kristo, nje ya Yesu Kristo huwezi kupata matokeo yanayokusudiwa, Mungu aliyemthibitisha Yesu kwa wanafunzi wake hawezi kumthibitisha kwa wasiomsikiliza au kumtii, kama tunataka kuona matokeo makubwa sana katika injili basi tumuhubiri Yesu Kristo:-

Filipo aliposhuka Samaria alimuhubiri Kristo na watu waliposikia waliponywa na kufunguliwa na kuokolewa - Matendo 8:5-8. “Filipo akatelemka akaingia mji wa Samaria, AKAWAHUBIRI KRISTO. Na makutano kwa nia moja WAKASIKILIZA maneno yale yaliyosemwa na Filipo walipoyasikia na kuziona ishara alizokuwa akizifanya. Kwa maana pepo wachafu wakawatoka wengi waliopagawa nao, wakilia kwa sauti kuu; na watu wengi waliopooza, na viwete, wakaponywa. Ikawa furaha kubwa katika mji ule.”

-          Ni Yesu Kristo pekee ndiye mwenye maneno ya uzima wa milele – watu wengi wanaweza kuwa na maneno ya Hekima “Falasafa”, lakini maneno hayo hayana uwezo wa kutoa uzima huu wala wa milele Yesu Kristo anayo maneno ya uzima wa milele, kila mtu anayemsikiliza anapewa uwezo wa kuwa na uzima wa milele

Yoahan 6:68-69 “Basi Simoni Petro akamjibu, Bwana! Twende kwa nani? Wewe unayo maneno ya uzima wa milele.Nasi tumesadiki, tena tumejua, ya kuwa wewe ndiwe Mtakatifu wa Mungu.”

-          Ni Yesu Kristo pekee ambaye anatajwa kuwa ndio njia na kweli na uzima, Mungu anataka watu wasimsikilize mwingine bali wamsikilize Yesu kwani wakimsikiliza yeye hawatapotea, Mungu hataki wanadamu wasikilize njia nyingine zinazopingana na Kristo au kuwaongoza kwenda upotevuni. Unataka uzima mwamini Bwana Yesu, mtii.

 Yohana 14:6 “Yesu akamwambia, Mimi ndimi njia, na kweli, na uzima; mtu haji kwa Baba, ila kwa njia ya mimi.”

-          Ni Yesu Kristo pekee ambaye amepewa mamlaka yote mbinguni na Duniani. Na jina kubwa kuliko majina yote iwe ni ya mbinguni au duniani uwezi kumfananisha Yesu Kristo na nabii mwingine yeyote, yeyote.

Mathayo 28:18 “Yesu akaja kwao, akasema nao, akawaambia, Nimepewa mamlaka yote mbinguni na duniani.”

Wafilipi 2:9-11 “Kwa hiyo tena Mungu alimwadhimisha mno, akamkirimia Jina lile lipitalo kila jina; ili kwa jina la Yesu kila goti lipigwe, la vitu vya mbinguni, na vya duniani, na vya chini ya nchi; na kila ulimi ukiri ya kuwa YESU KRISTO NI BWANA, kwa utukufu wa Mungu Baba.”     

Huyu ndiye Mwanangu mpendwa msikieni yeye.

Mathayo 17:1-5 “Na baada ya siku sita Yesu akawatwaa Petro, na Yakobo, na Yohana nduguye, akawaleta juu ya mlima mrefu faraghani; akageuka sura yake mbele yao; uso wake ukang'aa kama jua, mavazi yake yakawa meupe kama nuru. Na tazama, wakatokewa na Musa na Eliya, wakizungumza naye. Petro akajibu akamwambia Yesu, Bwana, ni vizuri sisi kuwapo hapa; ukitaka, nitafanya hapa vibanda vitatu, kimoja chako wewe, na kimoja cha Musa, na kimoja cha Eliya. Alipokuwa katika kusema, tazama, wingu jeupe likawatia uvuli; na tazama, sauti ikatoka katika lile wingu, ikasema, Huyu ni Mwanangu, mpendwa wangu, ninayependezwa naye; MSIKIENI yeye.”

Wakati Mungu anasema maneno haya ya muhimu sana mapema katika tukio hilo, Musa na Eliya walikuwa wameonekana wakizungumza na Yesu akiwa katikati yao, kimsingi Musa anawakilisha Sheria au Torati na Eliya anawakilisha Manabii, Katika hali ya sintofahamu Petro alitoa ushauri ambao Mbingu ziliukataa na kutamka maneno hayo mazito,  Petro alisema ni vema wakikaa hapo na vikajengwa vibanda vitatu kimoja cha Kristo, kingine cha Musa na kingine cha Eliya, unajua ni kwanini Petro alitamka haya katika mawazo yake alifikiri kuwa Musa na Eliya wako sawasawa na Yesu na hapo ndipo Mungu alipoingilia kati kumjulisha Petro na wenzake kuwa manabii hao ni tofauti na Bwana Yesu “HUYU NDIYE MWANANGU MPENDWA NINAYEPENDEZWA NAYE MSIKIENI YEYE” maneno haya yalikuwa yanafunua uwazi wa Mungu Baba kuwa Yesu ni mkuu kuliko Musa, Yesu ni mkuu kuliko Eliya, Yesu ni zaidi ya manabii wote, Yesu ndiye utimilifu wa Sheria na manabii, kwa hiyo yeye ndiye wa kusikilizwa, yeye ndiye wa kuaminiwa, yeye ndiye wa kumtii, yeye ndiye wa kufuata yeye ndiye wa kuyashika mafundisho yake, yeye ndiye mtekeleze maagizo yake, yeye ndiye wa kutegemewa, kumlinganisha Yesu na Musa ni sawa na kumlinganisha mtimishi mwaminifu na Mwana mwaminifu katika nyumba ya Mungu.

Waebrania 3:3-6 “Kwa maana huyo amehesabiwa kuwa amestahili utukufu zaidi kuliko Musa, kama vile yeye aitengenezaye nyumba alivyo na heshima zaidi ya hiyo nyumba. Maana kila nyumba imetengenezwa na mtu; ila yeye aliyevitengeneza vitu vyote ni Mungu. Na Musa kweli alikuwa mwaminifu katika nyumba yote ya Mungu kama mtumishi, awe ushuhuda wa mambo yatakayonenwa baadaye; bali Kristo, kama mwana, juu ya nyumba ya Mungu; ambaye nyumba yake ni sisi, kama tukishikamana sana na ujasiri wetu na fahari ya taraja letu mpaka mwisho.”                

Kwa msingi huo mtu awaye yote ambaye hatamsikiliza Yesu Kristo huyo atakatiliwa mbali na watu wake, ataangamia

Matendo 3:22-23 “Kwa maana Musa kweli alisema ya kwamba, Bwana Mungu wenu atawainulieni nabii, katika ndugu zenu, kama mimi; msikieni yeye katika mambo yote atakayonena nanyi.Na itakuwa ya kwamba kila mtu asiyemsikiliza nabii huyo ataangamizwa na kutengwa na watu wake.”

Kwa hiyo maneno HUYU NDIYE MWANANGU MPENDWA NINAYEPENDEZWA NAYE MSIKILIZENI YEYE  Ni tamko la mamlaka ya kimbinguni linalomtangaza Yesu Kristo kuwa ndiye Masihi na Mwokozi wa ulimwengu na hakuna nabii mwingine yeyote ambaye ni mkubwa au ana heshima kubwa kuliko yeye tena wala hakuna mbadala wake, huyu ndiye Alfa na Omega kwa hiyo wito huo haukuwa wa Petro, Yakobo na Yohana bali ulikuwa ni wito kwa ulimwengu mzima kwamba macho na masikio yetu, mioyo yetu, imani yetu na utii wetu uelekezwe kwa Yesu, Musa alielekeza watu kwa Yesu, Manabii wote walielekeza kwa Yesu, Mitume walimuhubiri Kristo, na Roho Mtakatifu anamshuhudia Kristo, kwa hiyo hili lilikuwa onyo pia la wazi kwa wanadamu kwamba ole wako umwanimi mwingine au atakayekuja nyuma ya Yesu na kujifanya ni nabii au mjumbe wa mwenyezi Mungu, ni ujumbe unaowasaidia wakristo kutambua wazi nani ni nabii wa kweli na nani ni nabii wa uongo. Ole wako umuhubiri Siddhartha Gautama Budha wa Budha, ole wako umuhubiri Guru Nanak wa Sikhism, Ole wako umuhubiri Lao Tzu wa Taoisim, Ole wako Umuhubiri Master Confucius, wa Confucianism, Ole wako umuhubiri Zoroaster wa Zoroastrianism, Ole wako umuhubiri Bahaulah wa Bahai, Ole wako umuhubiri Muhamad wa Uislamu, mitume na watumishi wa Mungu wa kweli wanamuhubiri Kristo, sisi tunamuhubiri Yesu Kristo ya kuwa ni Bwana, ni hatari sana kumlinganisha Yesu na wanafalasafa wengine duniani.

2Wakorintho 4:3-5 “Lakini ikiwa injili yetu imesitirika, imesitirika kwa hao wanaopotea; ambao ndani yao mungu wa dunia hii amepofusha fikira zao wasioamini, isiwazukie nuru ya injili ya utukufu wake Kristo aliye sura yake Mungu. Kwa maana hatujihubiri wenyewe, bali Kristo Yesu ya kuwa ni Bwana; na sisi wenyewe kuwa tu watumishi wenu kwa ajili ya Yesu.”

Na Rev. Innocent Samuel Kamote

Mkuu wa wajenzi mwenye Hekima.