Jumatatu, 30 Julai 2018

Furaha timilifu!

Mstari wa Msingi: Yohana 16: 23 -24 Tena siku ile hamtaniuliza neno lo lote. Amin, amin, nawaambia, Mkimwomba Baba neno lo lote atawapa kwa jina langu. Hata sasa hamkuomba neno kwa jina langu; ombeni, nanyi mtapata; FURAHA YENU IWE TIMILIFU.”

 Je wewe hutegemea hali ya nje kama chanzo cha Furaha maishani mwako? Angalia kwamba Mungu ndio chanzo kikubwa cha furaha timilifu na sio vinginevyo

Utangulizi:

Maisha ya mwanadamu yanategemea sana kuwa na furaha ili yawe maisha, na mwanadamu siku zote anafanya kila kitu kwaajili ya furaha yake tuu. Furaha ndio kilele cha maisha ya mwanadamu, kila analolifanya mwanadamu lengo lake kuu ni kupata furaha.

Mathalani ukitoa msaada kwa mtu moyo huwa na furaha, ukipongezwa au kusifiwa kwa jambo fulani moyo huwa na furaha, ukiwa mshika ibada moyo huwa na furaha, ukiwa na mke mwema au mume mwema moyo huwa na furaha vilevile, ukiwa na watoto wazuri na wenye adabu na kujiheshimu, ukifanya kazi kwa ufanisi, ukipata malipo ya kazi yako au mshahara moyo huwa na furaha kadhalika, ukisikiliza mziki au filam ama picha na hata kusoma vitabu moyo huwa na furaha pia, Ukiwa na mafanikio makubwa, ukijenga nyumba, ukiwa na mashamba, ukinunua gari, ukipandishwa cheo, ukichumbiwa, ukiolewa, ukizaa mtoto, ukiwa na afya njema moyo huwa na furaha, ukipewa tuzo, ukishinda uchaguzi, ukimiliki kampuni na kufanikiwa Moyo huwa na furaha Lakini pamoja na hayo yooote bado utaweza kuona kuwa hakuna furaha iliyo timilifu, Je ni wapi tunaweza kuona na kuwa na furaha timilifu? 

Furaha nini?

Ni vigumu sana kuielezea furaha zaidi ya neno lenyewe furaha, Katika kiingereza neno linalotumika kuelezea furaha ni “JOY” ambalo katika lugha ya kiyunani ni “CHARA” linatamkwa “KHA-RAH” ambalo maana yake ni Hali ya kujaa raha katika nafsi kutokana na kufikia au kufanikiwa katika jambo fulani, hali ya kuwa na raha isiyo na mipaka kutokana na kutoshelezwa kwa nafsi.

Katika imani ya Kikristo tunaweza kusema ni Raha ya nafsi ndani ya mwamini anayopipata kama matokeo ya Neema na upendo wa Roho Mtakatifu kumuwezesha mtu huyo, kufurahia kuwa na uhusiano na Mungu na kumjua Yesu Kristo, Neno lake na makusudi yake na tumaini lililo ndani yake.

Je ni watu wangapi wana furaha?

Ukiulizwa swali je una furaha je unaweza kulijibu vipi? Ni swali gumu sana, kwani unaweza ukawa una furaha lakini unafahamu kuwa furaha hiyo haidumu milele. Labda una furaha kutokana na kuwa una familia nzuri, lakini kwa kina utaona kuwa furaha hiyo inategemea uwepo wa familia nzuri, na uwepo huo ukitenganishwa kwa vifo, maisha, mabadiliko mbalimbali basi furaha yake nayo inaisha. Hivyo kuna furaha za milele na furaha ya muda mfupi.

Kila mtu anapenda kuwa na furaha, na lengo kuu la maisha ni kuwa na furaha. Hata hivyo furaha ya watu wengi sana sio furaha timilifu kwa sababu furaha zao zinatawaliwa na hali ya nje ya maisha yao angalia mfano huu:-

Mtu moja alikuwa anamiliki nyumba nzuri sana ni nyumba ya thamani na ilikuwa yenye kupendeza na yenye mvuto mkubwa sana katika mji aliokuwa anaishi, na jamaa huyu aliipenda nyumba yake sana watu wengi waliwahi kumuendea na kumuomba awauzie hata kwa bei kubwa mara mbili ya thamani yake lakini alikataa, wakati fulani bwana huyu alisafiri na aliporejea aliikuta nyumba yake ikiwa inawaka moto mkubwa sana na hivyo alipatwa na huzuni kubwa mno! Mamia ya watu walikusanyika kwaajili ya kuangalia namna ya kusaidia kuuzima moto ule, lakini hakuna walichofanikiwa kukiokoa katika moto ule

Mara mwanae mkubwa alimjia na kumnongoneza sikioni, Baba usiogope, “Niliiuza nyumba hii jana na niliiuza kwa bei nzuri sana, bei ilikuwa nzuri kiasi ambacho nisingeliweza kukusubiri au kukutaarifu, Hivyo unisamehe bure tu baba”

Baba yule alivuta pumzi na kuzishusha akimshukuru Mungu kwani sasa amekuwa moja ya washuhudiaji wa ajali ile kama walivyo wengine,

Mara mwanae wa pili alikuja mbio akimkimbilia na kumbwambia baba unafanya nini uangalia nyumba yetu ikiwa inaungua? Baba alimjibu kijana yule kuwa tulia kwani kaka yako aliiuza tayari kwa bei nzuri, Kija ayule alimwambia baba yake kuwa tulichukua kiwango fulani tu cha fedha na sio zote hivyo nina mashaka kama yule aliyenunua atakubali kumalizia ilihali nyumba imeungua!
Yule baba alianza kulia tena, machozi ambayo mwanzoni alikuwa ameshasahau,Moyo wake ulianza kwenda mbio sana na nguvu zikaanza kumuishia alikuwa mwenye huzini kubwa sana, Mara mtoto wake wa tatu akaja na kumwambie Baba yule mtu aliyenunua nyumba yetu ni mtu mwema na mwaminifu na mwenye kutunza sana ahadi kwani nimetoka kuongea naye sasa na ameniambia “ Haijalishi kwamba nyumba imeungua au la Nyumba ni yangu na nitalipa kiwango chote cha fedha tulichopatana, kwa kuwa hakuna aliyejua kuwa nyumba itaungua, Kisha wote wakasimama wakiwa wametulia kama washuhudiaji wengine wakiangalia nyumba inayoungua bila wasiwasi wowote!
Tunajifunza nini kutokana na kisa hiki? Watu wengi sana wanajisikia kuwa wenye furaha kutokana na hali ya nje ya mambo na sio ya ndani na kwa sababu hiyo hawawezi kuwa na furaha ya kweli, furaha ya kibinadamu ya ya dunia hii ni yenye kuyumba kutokana na hali halisi ya kubadilika badilika kwa mambo, aidha furaha ya kweli haipatikani kwa kuwakosea wengine.

Wako watu wengine wanafikiri kuwa watakuwa wenye furaha kwa sababu ya kukandamiza wengine, kuwatesa, kuwatendea vibaya, kuwashitaki, kuwasengenya, na kuwakosea ni muhimu kufahamu kuwa watu wote wanahitaji furaha kwa sababu hiyo kama huwezi kuwasaidia wengine kuwa wenye furaha basi jitahidi usiwe sababu ya huzuni zao, furaha ya kweli hua kwa kuhakikisha kuwa wengine wana furaha kama wewe na sio kuwakosea. 

Faida za kuwa na furaha timilifu

Kwa mujibu wa wataalamu wa maswala ya saikolojia wanaeleza kuwa furaha ina faida kubwa sana
Zikiwemo

a. Inakulinda na magonjwa ya Moyo
b. Inaimarisha kinga za mwili
c. Inatupilia nje mikandamizo ya mawazo katika maisha
d. Inakulinda dhidi ya Magonjwa
e. Inarefusha maisha

Kitaalamu hata utungiswaji wa Mimba hutokea siku ambayo wana ndoa wote wamefurahi
Unawezaje kuwa na Furaha timilifu?

Kaa katika uwepo wa Mungu Zaburi 16:11Utanijulisha njia ya uzima; Mbele za uso wako ziko furaha tele; Na katika mkono wako wa kuume Mna mema ya milele.” Unaweza kuona maneno Mbele za uso wako ziko furaha tele yanamaanisha mbele za uwepo wa Mungu “Presence” kuna furaha tele, Musa alikuwa ni mtu aliyependa kukaa katika uwepo wa Mungu, alikaa uweponi mwa Munngu kiasi ambacho hakusikia njaa kwa siku 40 na hata aliporejea uso wake ulikuwa unangaa’ kiasi ambacho watu walishindwa kumtazama Kutoka 34:29-35Hata ikawa, Musa aliposhuka katika mlima Sinai, na zile mbao mbili za ushuhuda zilikuwa mkononi mwa Musa, hapo aliposhuka katika mlima, Musa hakujua ya kuwa ngozi ya uso wake iling'aa kwa sababu amesema naye. Basi Haruni na wana wote wa Israeli walipomwona Musa, tazama, ngozi ya uso wake iling'aa; nao wakaogopa kumkaribia. Musa akawaita; Haruni na wakuu wote wa kusanyiko wakarudi kwake; Musa akasema nao. Baadaye wana wa Israeli wote wakakaribia; akawausia maneno yote ambayo BWANA amemwambia katika mlima Sinai. Na Musa alipokuwa amekwisha kusema nao, akatia utaji juu ya uso wake. Lakini desturi ya Musa ilikuwa alipoingia mbele za BWANA kusema naye, kuuvua huo utaji mpaka atoke; akatoka akawaambia wana wa Israeli maneno yote aliyoambiwa. Wana wa Israeli wakauona uso wa Musa ya kuwa ngozi ya uso wake Musa iling'aa; naye Musa akautia utaji juu ya uso wake tena, hata alipoingia kusema naye.”

Usitawaliwe na hali ya nje.

Habakuki 3:17-18Maana mtini hautachanua maua, Wala mizabibuni hamtakuwa na matunda; Taabu ya mzeituni itakuwa bure, Na mashamba hayatatoa chakula; Zizini hamtakuwa na kundi, Wala vibandani hamtakuwa na kundi la ng'ombe; Walakini nitamfurahia Bwana Nitamshangilia Mungu wa wokovu wangu.” Kwa mujibu wa Habakuki ni kuwa yeye atamfurahi Mungu bila kujali kuwa mtini haujachanua maua, au zabibu hazina matunda aku mzaituni haukuzaa au mashamba hayakutoa chakula au mazizi mifugo kutokuwa na kitu, Yeye bado atafurahi, hii ni wazi kuwa Mungu ndio chanzo cha furaha yetu na sio vinginevyo.

Dumu katika kuomba.

Kwa mujibu wa Yesu Kristo ukweli ni kuwa maombi yanasaidia kwa kiwango kikubwa sana kuketa firaha timilifu, kila amtu anapaswa kuomba, maombi ni muhimu sana, usiache kuomba Yohana 16: 23 -24Tena siku ile hamtaniuliza neno lo lote. Amin, amin, nawaambia, Mkimwomba Baba neno lo lote atawapa kwa jina langu. Hata sasa hamkuomba neno kwa jina langu; ombeni, nanyi mtapata; FURAHA YENU IWE TIMILIFU.”

Mwamini Mungu na Kumtegemea.

Warumi 15:13Basi Mungu wa tumaini na awajaze ninyi furaha yote na amani katika kuamini, mpate kuzidi sana kuwa na tumaini, katika nguvu za Roho Mtakatifu.”, Imani katika Mungu na kumtegemea yeye kunaweza kutupa furaha timilifu.

Watumikie wengine Watu wanaowatumikia wengine huwa na furaha sana Duniani.

Na Mkuu wa wajenzi mwenye Hekima.

Rev. Innocent Kamote

Jumatatu, 23 Julai 2018

Pesa Katika Mdomo wa samaki

Andiko: Mathayo 17:24-27

Hata walipofika Kapernaumu, wale watozao nusu-shekeli walimwendea Petro, wakasema, Je! Mwalimu wenu hatoi nusu-shekeli? Akasema, Hutoa. Naye alipoingia nyumbani, Yesu alitangulia kumwuliza, akisema, Waonaje, Simoni? Wafalme wa dunia hutwaa kodi ama ushuru kwa watu gani? Kwa wana wao au kwa wageni? Naye aliposema, Kwa wageni, Yesu alimwambia, Basi, kama ni hivyo, wana ni mahuru. Lakini tusije tukawakwaza, enenda baharini ukatupe ndoana, ukatwae samaki yule azukaye kwanza; na ukifumbua mdomo wake utaona shekeli ichukue hiyo ukawape kwa ajili yangu na kwa ajili yako.”



Utangulizi:

Ni muhimu kufahamu kwamba hapa duniani, kila mtu anahitaji fedha kwaajili ya kutimiza mahitaji yake, Bila fedha wakati mwingine ni vigumu kukidhi mahitaji yetu yote,kwa kadiri siku zinavyokwenda na hali ya uchumi inabadilika na kwa sababu hiyo fedha inazidi kuwa ngumu sana, na maisha yanabadilika mno na kwa sababu hiyo fedha zinahitajika ili wana wa Mungu wasiweze kukudhalilisha, kutokana na kukosekana kwa fedha,

Yesu anatoa suluhu namna ya kupata fedha katika muujiza huu
Muujiza wa Yesu, kumtuma Petro kuvua samaki na kupata fedha unaonekana kutajwa katika Injili ya Mathayo pekee, penginepo kwa vile yeye alikuwa mtoza ushuru, ingawa watoza ushuru hawa hawakuwa mawakili ya serikali ya Rumi bali walikuwa watoza ushuru kwaajili ya ujenzi wa Hekalu.
Watoza ushuru wa Hekalu walimuuliza Petro kama Mwalimu nwao analipa kodi ya hekalu nae aliwajibu kuwa analipa,Petro aliporejea Yesu alizungumza naye kuhusu swala aliloulizwa kuhusu kodi

Naye alipoingia nyumbani, Yesu alitangulia kumwuliza, akisema, Waonaje, Simoni? Wafalme wa dunia hutwaa kodi ama ushuru kwa watu gani? Kwa wana wao au kwa wageni? Naye aliposema, Kwa wageni, Yesu alimwambia, Basi, kama ni hivyo, wana ni mahuru.” Yesu alikuwa akimaanisha wao kama wana wa Mungu wako huru wasingelipaswa kulipa kodi ile, lakini ili aiwakwaze watoza ushuru, Yesu alitoa maagizo kwa Petro nini anapaswa kufanya ili kukidhi hitaji hilo la kulipa kodi, tunaona Yesu akimuelekeza Petro kwenda kutupa Ndoana na kuvua samaki na samaki yule wa Kwanza angekuwa na fedha ambayo ingetosha kulipa Kodi yake na Petro. Watu wengi na walimu wengi wa neno la Mungu hawasemi mengi kuhusu muujiza huu,

Lakini mimi naona yako mambo ya kujifunza katika muujiza huu
1. Wote tunahitaji fedha kwaajili ya kukidhi mahitaji mbalimbali tuliyonayo katika Maisha
2. Wote tunahitaji fedha kwaajili ya kumuabudu Mungu na kumtumikia
3. Wote tunahitaji fedha kwaajili ya kulipia ada za shule za vijana wetu
4. Wote tunahitaji fedha kwaajili ya hatima ya wale wanaotuzunguka na wanaotutegemea
5. Wote tunahitaji fedha kwaaji ya kujiwekea hadhina mbinguni, tunapomtolea yeye na kuwapa wajane na masikini, na kutunza wazee wetu, na kuukuza ufalme wa Mungu.

Kama Petro na Mwalimu wake hawangelipa Kodi hii wangedhalilika, watu wangemsema Yesu, kuwa anajifanya mtu wa Mungu lakini halipi kodi ya Hekalu, hivyo Yesu anatambua kuwa watoto wake wanapokosa fedha wanadhalilika, wanaingia katika fadhaa, na hivyo alimuelekeza Petro nini cha kufanya.

Yesu alifanya Muujiza huu kuonyesha kuwa ana nguvu dhidi ya Fedha, “Jesus Has power over money” Yeye anauwezo juu ya fedha, Tatizo kubwa la watu wengi wa Mungu leo hawajawahi kumuambia Yesu kuwa wanashida ya fedha, linapokuja tatizo la fedha haraka sana hapo ndipo watu wengi sana hutumia akili na kuanza kusugua vichwa vyao, sio tu kusugua vichwa pia huanza kuumia moyo, na kuingia hofu na hata kulalamika, Tumesahau kabisa kuwa Mungu wetu anauwezo wa kutusaidia kama alivyomfanyia Petro .

Ni muhimu kufahamu kuwa Yesu ana uwezo juu ya fedha, Biblia inaeleza wazi kuwa yeye ingawa alikuwa tajiri alifanyika Masikini ili sisi tuwe matajiri 2Wakoritho 8:9 “Maana mmejua neema ya Bwana wetu Yesu Kristo, jinsi alivyokuwa maskini kwa ajili yenu, ingawa alikuwa tajiri, ili kwamba ninyi mpate kuwa matajiri kwa umaskini wake.”

Biblia inatufundisha kuwa ni yeye anayetupa nguvu ya kupata utajiri Kumbukumbu 8:18 “Bali utamkumbuka Bwana, Mungu wako, maana ndiye akupaye nguvu za kupata utajiri; ili alifanye imara agano lake alilowapa baba zako, kama hivi leo.”

Biblia inaonyesha kuwa Petro alikuwa na uhitaji na hivyo huenda alimtaarifu Yesu kilichotokea, kwa ufupi alimuomba, kuhusu uhitaji wa kulipa kodi kwamba wanadaiwa kodi, na Yesu alijibu maombi hayo, kwa msingi huo kama tunavyoomba kwaajili ya mahitaji mengine tunahitaji pia kumuomba Mungu atupe fedha ili tusidhalilike.

Biblia inasema Hamna kitu kwa sababu hamwombi ni lazima tumuombe Mungu kwaajili ya hali ya uchumi wa familia zetu na mahitaji yetu, Sala ya Bwana inasema utupe leo riziki yatu ya kila siku, riziki yetu ya kila siku haiwezi kupatikana bila kuhusisha fedha je tumewahi kuomba fedha?

labda wengi tumefungwa na ile dhana ya fundisho la shina la mabaya yote ni kupenda fedha, lakini biblia inamaanisha kupenda fedha kuliko Mungu, na haimaanishi kuwa watu wake hawahitaji fedha, hapa mimi nazungumzia ule uhitaji fedha wa kawaida, kama ilivyokuwa kwa Petro anadaiwa kodi, labda huenda na wewe unadaiwa kodi ya nyumba, ama una madeni, ama unadaiwa ada ya watoto wako na kadhalika haja za namna hii ni vema pia Mungu akazijua, wengi hunijia wakitaka maombezi ya namna mbalimbali, lakini sijawahi ona mtu akinijia kuomba maombi apate fedha, wengi linapokuja swala la uhitaji wa kifedha, wanatumia akili zao wenyewe na wanaishia kupata msongo wa mawazo, huku haja hiyo ikiwa haijawasilishwa kwa Mungu, kutokumwambia Mungu uhitaji wetu wa kifedha ni daharau, ni sawa na kufikiri kuwa labda swala la kupata fedha Mungu haliwezi, lakini maandiko yanasemaje yote yawezekana kwa Mungu. kwa nini unasumbuka hali neno la Mungu linasema

Wafilipi 4: 6 maandiko yanasema “Msijisumbue kwa neno lo lote; bali katika kila neno kwa kusali na kuomba, pamoja na kushukuru, haja zenu na zijulikane na Mungu.”

Je umewahi kumuomba Mungu waziwazi kwamba akupatie fedha ? umewahi kumuombea Mumeo, mkeo, wazazi, ndugu zako wawe na upenyo wa kifedha? Lazima tumuombe Mungu katika hitaji hili.

Mathayo 7: 7-11 Biblia inatukumbusha kuwa, Mungu ni Baba mwenye upendo ambaye huwapa watoto wake Mahitaji kwa kadri walivyoomba.

Anauliza je ni nani kati yenu mwanaye akiomba mkate atampa Jiwe? Au akiomba samaki atampa nyoka? Nauliza umewahi kumuomba Mungu akupe fedha ? au umetamani tu kuwa na fedha kwa kutumia akili zako mwenyewe bila kumwambia Mungu

Anamalizia kwa kusema " kama ninyi mlio waovu mwaweza kuwapa watoto wenu vipawa vyema je si zaidi sana Baba yenu Wa Mbinguni .........'' Hivyo kile tunachokiomba ndicho tutakachopokea.

1 Petro 5: 7 maandio yanasema wazi kuwa, Mungu hujishughulisha Zaidi na Mambo Yetu na hivyo tumpe yeye Fadhaa/haja zetu.

Anasema.
7 huku mkimtwika yeye fadhaa zenu zote, kwa maana yeye hujishughulisha sana kwa mambo yenu.
Kama utasema hujui namna ya kuomba hususani kuomba fedha kwa Mungu basi fuata muongozo wa mambo ya kuombea:-

Mambo ya kuombea:
• Omba Mungu akuweke mbali na Madeni, Yesu na Petro hapa walikuwa wanadaiwa kodi ya hekalu. na petro alipatwa na fadhaa
• Omba Mungu akusaidie usiwe mzigo kwa wazazi wako
• Omba Mungu kwamba akupe fedha nyingi kuliko matumizi
• Omba Mungu kwamba uwe na uwezo wa kukopesha na sio kukopa
• Vunja roho ya umasikini, kataa mikosi inayoendana na kipato chako
• Kataa roho ya umasikini na magonjwa na masumbufu
• Kemea Roho za wizi, hasara, mikosi, chuma ulete, kukopera na jicho baya, Mwambie Mungu akupatie ulinzi wa kutoshja katika mali zako.

Mwambie Mungu atumie ujuzi aliokupa au atakaokupa kukupa fedha

Yesu alitumia ujuzi aliokuwa nao Petro, kumpatia fedha, Petro alikuwa Mvuvi kabla ya kumtumikia Mungu, kwa kuwa mwanafunzi wa Yesu. Hivyo Yesu alitumia ujuzi na kipawa alichokuwa nacho ili kupata fedha ya kulipa kodi. alimuagiza aende akavue samaki na muujiza ulikuwa ndani ya samaki wa kwanza atakayevuliwa, kumbe fedha zetu ziko katika midomo ya samaki, ni lazima twende kwenye ujuzi ule tulionao tuweze kuzitoa fedha zetu huko na kukidhi mahitaji yetu tuliyo nayo
Fanya kazi kwa bidii, ile kazi aliyokupa Mungu fanya kwa uaminifu, fanya kama unamtumikia Mungu yeye anasema atazibariki kazi za mikono yako.

Yesu hakumwambia Petro akacheze Biko wala tatu mzuka hii ni michezo ya watu waliokata tamaa, wanaishi kwa kubahatisha, ni michezo ya watu masikini, wanaoishi kwa ndoto za mchana, wakitarajia kitu kutoka kwa miungu ya bahati nasibu, Mungu hajatuleta duniani ili tuishi maisha ya kubahatisha kanuni kuu za mafanikio ziko katika kazi naujuzi au kipawa ulichopewa na Mungu huko ndioko pesa yako iliko,

Biblia inatutaka tufanye kazi kwa bidii, Pesa iko katika mdomo wa samaki. Lakini ni lazima ukavue, ukienda kuvua samaki yule utakayemvua ana pesa mdomoni mwake, za kukidhi mahitaji yako ya ya jamaa zako, Nikutakie uwajibikaji mwema na Mungu aibariki kazi ya mikono yako Amen. Nakukumbusha kuwa fedha yako iko katika midomo ya samaki endenda ukatupe ndoana.

Na.Rev. Innocent Kamote
 
Mkuu wa wajenzi mwenye Hekima.

Jumapili, 15 Julai 2018

Enyi kizazi kisichoamini!

Mathayo 17:14-20Nao walipoufikia mkutano, mtu mmoja akamjia, akampigia magoti, akisema, Bwana, umrehemu mwanangu, kwa kuwa ana kifafa, na kuteswa vibaya; maana mara nyingi huanguka motoni, na mara nyingi majini. Nikamleta kwa wanafunzi wako, wasiweze kumponya. Yesu akajibu, akasema, ENYI KIZAZI KISICHOAMINI, kilichopotoka, nitakaa pamoja nanyi hata lini? Nitachukuliana nanyi hata lini? Mleteni huku kwangu.  Yesu akamkemea pepo, naye akamtoka; yule kijana akapona tangu saa ile. Kisha wale wanafunzi wakamwendea Yesu kwa faragha wakasema Mbona sisi hatukuweza kumtoa? Yesu akawaambia, Kwa sababu ya upungufu wa imani yenu. Kwa maana, amin, nawaambia, Mkiwa na imani kiasi cha punje ya haradali mtauambia mlima huu, Ondoka hapa uende kule; nao utaondoka; wala halitakuwako neno lisilowezekana kwenu.” 



Imani binafsi ambayo haionekani kufanya kitu wakati wa matatizo hiyo sio Imani sahihi –W. Willberfoce

Utangulizi:

Mungu anamtarajia kila mwanadamu, aliyeitwa naye kuwa mwenye uwezo wa kuleta suluhu kwa matatizo yanayoizunguka jamii yake, Kusudi kubwa la Mungu kulichagua kanisa ilikuwa ili kanisa liweze kuwa na majibu ya changamoto zote katika jamii, Mungu anataka watu wenye uhodari, wanaoweza kutatua matatizo yanayoikabili jamii, alipokaa na wanafunzi wake alikuwa na matarajio ya jinsi hii hii, Lakini kama ilivyo kwa jamii ya leo na kanisa la leo, Wanafunzi wake pia walishindwa kutatua na kumaliza changamoto zilizowasilishwa kwao na mtu mmoja katika jamii. 
       
Katika Mistari ya msingi tunaona Wanafunzi wa Yesu wanaletewa kijana wa Pekee na Mzee mmoja, kijana huyu anateswa na Mapepo na kumtupa kila wakati, na ni lazima alimjeruhi, Baba wa mtoto ameingiwa na mashaka makubwa kwani anakosa tumaini anaona atapoteza kijana wake wa pekee ambaye shetani anamsumbua, Swala hili linatokea kuwa kitu cha kusikitisha kwa wanafunzi wa Yesu na inakuwa ni aibu kuwa wanashindwa kutatua tatizo hili, Yesu hakuweko karibu wakati huu alikuwa pamoja na wanafunzi watatu Petro, Yakobo na Yohana,  Hivyo wanafunzi tisa wanajaribu kutoa pepo wanashindwa hii ilikuwa mbele ya umati mkubwa wa watu, Tatizo halikuwa jipya kwa vile Walikutana na changamoto kama hii na Yesu aliitatua  

Marko 1:23-27Na mara palikuwapo ndani ya sinagogi lao mtu mwenye pepo mchafu; akapaza sauti, akisema, Tuna nini nawe, Yesu wa Nazareti? Je! Umekuja kutuangamiza? Nakutambua u nani, Mtakatifu wa Mungu. Yesu akamkemea, akisema, Fumba kinywa, umtoke. Yule pepo mchafu akamtia kifafa, akalia kwa sauti kuu, akamtoka. Wakashangaa wote, hata wakaulizana, wakisema, Nini hii? Ni elimu mpya! Maana kwa uweza awaamuru hata pepo wachafu, nao wamtii!”  na pia Marko 5:1-9Wakafika ng'ambo ya bahari mpaka nchi ya Wagerasi. Na alipokwisha kushuka chomboni, mara alikutana na mtu, ambaye ametoka makaburini, mwenye pepo mchafu;  makao yake yalikuwa pale makaburini; wala hakuna mtu ye yote aliyeweza kumfunga tena, hata kwa minyororo;kwa sababu alikuwa amefungwa mara nyingi kwa pingu na minyororo, akaikata ile minyororo, na kuzivunja-vunja zile pingu; wala hakuna mtu aliyekuwa na nguvu za kumshinda. Na sikuzote, usiku na mchana, alikuwako makaburini na milimani, akipiga kelele na kujikata-kata kwa mawe. Na alipomwona Yesu kwa mbali, alipiga mbio, akamsujudia;  akapiga kelele kwa sauti kuu, akasema, Nina nini nawe, Yesu, Mwana wa Mungu aliye juu? Nakuapisha kwa Mungu usinitese. Kwa sababu amemwambia, Ewe pepo mchafu, mtoke mtu huyu.  Akamwuliza, Jina lako nani? Akamjibu, Jina langu ni Legioni, kwa kuwa tu wengi” 

Lakini vilevile Yesu alishawapa Mamlaka ya kufanya kazi hii Mathayo 10:1, Lakini hapa wanashindwa, Yesu anatokea na kila mmoja ana furaha kwani Yesu aliweza kutatua tatizo, lakini wanafunzi wa Yesu hawakuweza kutatua tatizo lililokuweko, Swali kuu linazaliwa nao, Yesu anajibu kwa kukemea Enyi kizazi kisichoamiana. 

Kwanini sisi hatukuweza kumtoa? 

Yesu hakuwaambia kuwa tatizo liko kwenye mioyo yenu, Tatizo haikuwa kwamba kuna kanuni fulani haijatumika, Maana wengine mpaka wayaimbie Pambio mapepo kwanza, Tatizo sio kuwa hawakuwa na bidii, au kuwa hawana uzoefu, au hawakujaribu sana, wala sio kwa sababu hawakuwa na nguvu za uuongu ndani yao hapana, Yesu anawaambia ni” kwa sababu ya Upungufu wa Imani yenu” 

Math 17:20 “Yesu akawaambia, Kwa sababu ya upungufu wa imani yenu. Kwa maana, amin, nawaambia, Mkiwa na imani kiasi cha punje ya haradali mtauambia mlima huu, Ondoka hapa uende kule; nao utaondoka; wala halitakuwako neno lisilowezekana kwenu.”

Kanisa linapaswa kuelewa kanuni za utendaji wa Mungu

1.       Mungu hufanya miitikio yeke kwa Mtu anayemwamini, watu wanaomwamini Mungu wanaitwa “Risk takers” watu wenye uwezo wa kufanya maamuzi magumu, ni wenye ujasiri wa kutatua matatizo pasipo hofu ni watu ambao hawana shaka ni watu ambao wanamuamini Mungu na uwezo wake na hivyo kuchukua hatua za hatarishi, Ibrahimu, Musa, Joshua, Daniel na wengine wote walimuamini Mungu Waebrania 11:6 Pasipo imani haiwezekani kumpendeza Neno la Mungu linasema Waebrania 11:6 “Lakini pasipo imani haiwezekani kumpendeza; kwa maana mtu amwendeaye Mungu lazima aamini kwamba yeye yuko, na kwamba huwapa thawabu wale wamtafutao.”

2.       Mungu anataka tumuamini na kumtegemea Kama tunataka kuona kazi zake zikitendeka 

kwetu haijalishi tatizo ni baya kiasi gani au kubwa kiasi gani lakini nini kinaendelea moyoni mwako? Kinachoendelea ndani yako ni cha muhimu kuliko kinachotokea nje yako, Moyo wako unakuawaje unapokutana na changamoto, je unaogopa? Au una ujasiri ukijua kuwa Mungu yuko pamoja nawe hupaswi kuogopa, Yesu hajali ukuu wa tatizo, kuwa limeanza tangu utoto, au ni la ukoo mzima au limelishinda taifa zima Yesu haogopi hilo wala haangalii hilo, haijalishi Madaktari wanasemaje, Mzee alipomuona Yesu alimwambia ukiweza unaweza kutusaidia, Yesu alishangazwa na mashaka makubwa aliyokuwa nayo baba yule, kweli ilikuwa ni kizazi kisichoamini, Ukiweza? Yesu alimjibu Yote yawezekana kwake aaminiye Marko 9:22-23 “Na mara nyingi amemtupa katika moto, na katika maji, amwangamize; lakini ukiweza neno lo lote, utuhurumie, na kutusaidia. Yesu akamwambia, Ukiweza! Yote yawezekana kwake aaminiye”.

3.       Mzee aliomba Naamini nisaidie kutokuamini kwangu, zinapotokea changamoto, hatupaswi kuangalia ukubwa wa changamoto,  uweza wa changamoto au muda wa changamoto bali tunapaswa kumsihi Mungu atuongezee imani aondoe mashaka ndani yetu, wakati tunapokabiliana na changamoto zozote acha kuwaangalia wanadamu, acha kuangalia ukubwa wa tatizo, acha kuangalia umati wa watu, acha kufadhaika Muamini Mungu muamini na Bwana Yesu kila kitu kitakuwa shwari.

4.       Ni imani kiasi gani inahitajika kwetu? Kimsingi kwa vile tatizo lilikuwa kubwa na lina historia ya kutisha basi wanafunzi walifikiri wanahitaji kuwa na imani kubwa sana  na hivyo labda jibu sahihi la Yesu lingekuwa kwamba kwa vile tatizo ni kubwa basi mnahitaji imani kubwa sana au kuongezewa imani, Lakini ni dhahiri wanafunzi wa Yesu na hata mzee yule hawakuwa na imani kabisa, walijifikiri kuwa wao ni watu maalumu, Yesu alisisitiza kuwa na imani na sio kuhusu size au kipimo cha imani, Ni lazima tumuamini Mungu kwa kiwango cha juu sana na kuacha kujiamini sisi, tusiangalie umaarufu wa dhehebu letu, muda wa kutembea na Yesu, umaalumu wa aina ya huduma uliyo nayo, uzoefu katika huduma, uwezo wetu wa kumtii Mungu au sheria za Mungu bali namna na jinsi unavyomtegemea Mungu chini ya neema yake, Lazima tumwangalie yeye kwa kuwa yeye Hashindwi kitu Luka 1:37 “kwa kuwa hakuna neno lisilowezekana kwa Mungu.”

Enyi Kizazi kisichoamini.

Mara nyingi tunaweza kuona kuwa kuna tofauti kubwa kati ya kizazi kilichopita na kizazi cha leo kwa sababu ya imani, Inaonekana kama Mungu aliwatumia sana wazee wetu kuliko anavyotumia watu leo, Matamanio ya Mungu ni kuona watu wakimtumaini Mungu kwa uzito zaidi nyakati za leo na kutumiwa na Mungu kwa kiwango kikubwa katika nyakati za leo kuliko zamani, lakini shida Kubwa ni Hiki kizazi kisichoamini, Yesu alikemea Enyi Kizazi kisichoamini, Mungu anajua kuwa matatizo ya dunia hii na shuda zinazoukabili ulimwengu zinaweza kutatuliwa na watu waliamuamini na wanaomtumaini Mungu sio katika kutoa pepo tu bali kutatua matatizo ya wanadamu. 

-          William Wilberforce –  Alizaliwa 24 August 1759 – 29 July 1833 alikuwa mwanasiasa huko Uingereza na alijulikana kama kiongozi mwenye ushawishi aliyeendesha mpango wa kukomesha Biashara ya utumwa, alikuwa ni mbunge wa jimbo la Yorkshire kati ya mwaka 1784 – 1812, mwaka 1785 aliokoka na kumuamini Yesu kuwa Bwana na Mwokozi, jambo ambalo lilimpelekea kubadilika kabisa katika mtazamo wake wa maisha  na kusukumwa katika kupinga na kukomesha biashara ya utumwa, alipata elimu yake katika chuo cha ST Johns College cha Cambridge. 

-          Elisha aliweza kutatua Matatizo ya Mjane mmoja katika jamii yake na kukomesha kabisa tatizo lililokuwepo kwa Neema ya Mungu “ 2Wafalme 4:1-7” 

-          Dunia ina matatizo Mengi yanayohitaji ufumbuzi leo, Utunzaji wa Mazingira, Matumizi  mazuri ya ardhi, uwepo wa kemikali hatarishi, ugaidi, magonjwa, umasikini, shida za kisiasa, uongozi, uchumi, maji, ukame, ubaguzi, mauaji, kutekwa, ujangili, wizi, ujambazi, uchawi, uadui, Mafarakano, talaka, watoto wa mitaani, Elimu duni, picha za ngono, na kadhalika, Yesu anataka watu wote wamuamini Mungu na kutumia uhusiano walio nao nay eye kwa imani katika kutatua matatizo ya watu, Hatuwezi kumtumia yesu Kristo kwa kutafuta umaarufu naye akakubali, Kila msomi anayesoma shule ya seminary anapaswa kuwa mtu atakayekuja kutatua matatizo ulimwenguni na kuleta mabadiliko kwa jina la Yesu.

Na mkuu wa wajenzi mwenye Hekima 
Rev. Innocent Kamote 

Jumapili, 1 Julai 2018

“Imeandikwa Mtu hataishi kwa Mkate tu”


Andiko la Msingi: Mathayo 4:3-4Mjaribu akamjia akamwambia, Ukiwa ndiwe Mwana wa Mungu, amuru kwamba mawe haya yawe mikate. Naye akajibu akasema, Imeandikwa, Mtu hataishi kwa mkate tu, ila kwa kila neno litokalo katika kinywa cha Mungu”.



Utangulizi:

Ni muhimu kufahamu kuwa Katika majaribu ambayo Yesu amewahi kupitia, Jaribu la kugeuza mawe kuwa mkate lilikuwa limekaa vizuri sana katika kumtega Bwana Yesu ili atende dhambi, Jaribu hili ndilo ambalo lilikuwa na uwezo mkubwa sana wa kufanikiwa, kwa sababu Yesu alikuwa amethibitishwa wazi  na hadharani tena na Mungu mwenyewe kuwa yeye ni Mwana wa Mungu Mathayo 3:17na tazama, sauti kutoka mbinguni ikisema, Huyu ni Mwanangu, mpendwa wangu, ninayependezwa naye. Na Hapa ni kama anapewa wakati muafaka na mzuri wa kuonyesha kwamba yeye kweli ni mwana wa Mungu ulikuwa ni wakati sahihi kabisa kwanza kumuonyesha shetani kuwa yeye ni nani, pili alikuwa na njaa tena amechoka,tena ana uhitaji, tena yuko peke yake, tena masikini, na ana uwezo wa kufanya muujiza na zaidi ya yoteni Mwana wa Mungu na uhitaji ulikuweko ilikuwa ni kama ujinga kwamba hutumii mamlaka kubwa uliyonayo hivi ndivyo shetani alivyokuwa akimjaribu Yesu, Yesu kama mwana wa Mungu ilikuwa ana wajibu wa kutoa amri tu au kutamka neno tu na kuonyesha nguvu zake na angefanya kusingelikuwa na tatizo.

Yesu alikuwa na uelewa Mkubwa sana alitambua kabisa kuwa anajaribiwa kama Adamu wa Kwanza, Ili apoteze kibali kwa Mungu, Yesu alijua kuwa anapaswa kulitii Neno la Mungu, na kufuata maelekezo ya Roho Mtakatifu Mpaka dakika ya mwisho, kwa vile ndiye aliyemuongoza ili ajaribiwe, Kama Yesu angeshindwa wokovu ungekuwa wa taabu sana, Utii wake ulikuwa unapimwa kama ulivyopimwa wa Adamu, Adamu alishindwa kulitii neno la Mungu, na hivyo akaleta mauti, Yesu aliweza kulitii neno la Mungu na hivyo akaletauzima

Jibu la Yesu kwa kweli lilikuwa tamu sanaNaye akajibu akasema, Imeandikwa, Mtu hataishi kwa mkate tu, ila kwa kila neno litokalo katika kinywa cha Munguwote tunafahamu umuhimu wa Chakula kwamba hakuna uhai bila kula, tunajua kuwa hatuwezi kustahimili maisha na shughuli zetu za kila siku bila chakula, au maswala yanayotupatia Chakula, Lakini Yesu alionyesha kuwa Mwanadamu hataishi kwa chakula tu, kuna jambo lingine muhimu zaidi ambalo ni neno la Mungu, ni muhimu tu kujiuliza kwa nini neno la Mungu ni Muhimu? Kuliko chakula?

1.       Neno la Mungu lina Nguvu, lina uwezo mkubwa sana kama Moto na uwezo mkubwa sana kama nyundo ya kuvunjia mawe Yeremia 23:28-29 “Nabii aliye na ndoto, na aseme ndoto yake; na yeye aliye na neno langu, na aseme neno langu kwa uaminifu. Makapi ni kitu gani kuliko ngano? Asema Bwana.  Je! Neno langu si kama moto? Asema Bwana; na kama nyundo ivunjayo mawe vipande vipande?Mungu anaonyesha ya kuwa Neno lake lina nguvu, ili maisha yetu yaweze kufanikiwa ni muhimu kuzungumza neno katika kila aina ya jaribu na mapito tunayoyapitia, tafuta neno la Mungu na lizungumze katika hali yoyote inayokukabili, tunaweza kuikabili haliyoyote ile katika kwa kulitamkia neno.

2.       Neno la Mungu ni Upanga wa kiroho Waebrania 4:12 “Maana Neno la Mungu li hai, tena lina nguvu, tena lina ukali kuliko upanga uwao wote ukatao kuwili, tena lachoma hata kuzigawanya nafsi na roho, na viungo na mafuta yaliyomo ndani yake; tena li jepesi kuyatambua mawazo na makusudi ya moyo.”Neno la Mungu linasifiwa hapa kuwa lina UHAI, LINA MGUVU, KALI KULIKO UPANGA UKATAO KUWILI,LINACHOMA, LINAWEZA KUGAWANYA NAFSI, ROHO, VIUNGO, NA MOYO  Hivyo linaweza kutumika kuzima mishale yote ya adui na kila elimu inayojiinua na Elimu ya Utukufu wa Mungu

3.       Neno la Mungu ni kweli, Ukweli ni silaha yenye nguvu kuliko silaha zozote, Shetani hutumia uongo kutushambulia lakini kweli ina nguvu, kweli ni silaha kuu kwa mujibu wa Maandiko,Waefeso 6:10-14 “Hatimaye, mzidi kuwa hodari katika Bwana na katika uweza wa nguvu zake. Vaeni silaha zote za Mungu, mpate kuweza kuzipinga hila za Shetani. Kwa maana kushindana kwetu sisi si juu ya damu na nyama; bali ni juu ya falme na mamlaka, juu ya wakuu wa giza hili, juu ya majeshi ya pepo wabaya katika ulimwengu wa roho. Kwa sababu hiyo twaeni silaha zote za Mungu, mpate kuweza kushindana siku ya uovu, na mkiisha kuyatimiza yote, kusimama. Basi simameni, hali mmejifunga kweli viunoni, na kuvaa dirii ya haki kifuaniKama tunataka kuwa washindi wakati wote na kupata matokeo yaliyo thabiti hatuna budi kuhakikisha kuwa tunasimama katika kweli ya Neno la Mungu, Neno la Mungu lina uwezo wa kutakasa na kumfanya mtu wa Mungu akamilike Yohana 15:3,  17:17

4.       Neno la Mungu ni Roho tena ni uzima Yohana 6:63 “Roho ndiyo itiayo uzima, mwili haufai kitu; maneno hayo niliyowaambia ni roho, tena ni uzima.”Yesu alikuwa akimaanisha kuwa Neno analotupa yeye lina uzweza linanufaisha roho na sio mwili, Torati ya Musa ilikuwa na manufaa ya kimwili lakini Maneno na mafundisho ya Kristo yana nufaisha roho yana uzima ndani yake, Biblia inaonyesha ya kuwa kila kitu kitapia lakini neno la Mungu litasimama milele, ni neno la Milele, Kila mtu anayetaka kufanikiwa katika jambo lolote anapaswa kuliishi neno, kuliangalia neno, kulitazama neno, katika mazingira yoyote ishi kwa neno, Acha kuangalia nafasi uliyonayo, uanafunzi ulionao, cheo ulicho nacho akili ulizo nazo, Uzima wetu umewekwa katika neno, likitumika kwa halali shetani anajua kuwa lina nguvu na analiogopa neno.

Hitimisho:
Kama Yesu angetii maneno ya shetani na kugeuza mawe kuwa mkate maana yake angekuwa amelikataa neno la Mungu sawa na adamu na angekuwa ameyakubali maneno ya shetani kama Eva
Kila mmoja wetu anapaswa kuishi sawasawa na neno la Mungu, kila siku hatuna budi kuishi na sawa na neno la Mungu, Chakula cha siku moja tu kinatosheleza mahitaji ya mwili usio wa Milele lakini neno la Mungu linautoshelevu wa milele, Liseme neno. Liishi neno. Lihubiri neno litumikie neno, litendee kazi neno, liamini neno, litumie neno la MUngu na utaona faida kubwa sana katika maisha yetu, Mtu hataishi kwa Mkate tu Bali kwa kila neno litokalo katika Kinywa cha Mungu.

Ushindi wa Yesu Kristo ulitokana na ufahamu wa neno, maisha yetu na mafanikio yetu yamefungwa katika neno Yoshua 1:5-8 Biblia inasema “Hapatakuwa mtu ye yote atakayeweza kusimama mbele yako siku zote za maisha yako; kama nilivyokuwa pamoja na Musa, ndivyo nitakavyokuwa pamoja na wewe; sitakupungukia wala sitakuacha. Uwe hodari na moyo wa ushujaa, maana ni wewe utakayewarithisha watu hawa nchi hii niliyowaapia baba zao ya kwamba nitawapa. Uwe hodari tu na ushujaa mwingi, uangalie kutenda sawasawa na sheria yote aliyokuamuru Musa mtumishi wangu; usiiache, kwenda mkono wa kuume, au wa kushoto, upate kufanikiwa sana kila uendako. Kitabu hiki cha torati kisiondoke kinywani mwako, bali yatafakari maneno yake mchana na usiku, upate kuangalia kutenda sawasawa na maneno yote yaliyoandikwa humo; maana ndipo utakapoifanikisha njia yako, kisha ndipo utakapositawi sana.”  
          
Na mkuu wa wajenzi mwenye Hekima!

Rev. Innocent Kamote.