Jumapili, 19 Aprili 2015

Umuhimu Wa Kuabudu !



 Amini usiamini mpenzi kama kuna jambo la msingi na la muhimu Duniani ambalo mkristo anaweza kulifanya ni swala la kuabudu, Hili ni jambo ambalo linaweza kufanywa  na Mkristo Binafsi au na wenzake kuinuia juu mioyo yao na kumuhimidi Mungu  wa mbinguni, Kuabudu ndio kiini kikuu cha kuweko kwa mwanadamu, Ni jambo ambalo liko katika Hisia, moyo, mawazo na shauku ya mwanadamu, Hakuna mahali duniani ambako hakuna binadamu asiye na kiu au shauku ya kuabudu hali hii ni shauku ya wanadamu ya kimaumbile kujibu hisia za upendo wa Mungu alionao kwa mwanadamu

      Kumuabudu Mungu na kumuhimidi Yeye na kujitoa kwake kunainua juu uwezo wa mkristo na mwanadamu kujimimina kihisia na kufurahia uhusiano wake na Mungu, kila mkristo ni lazima akubaliane nami kuwa kuabuni ni muhimu na ni lazima, Hakuna kanisa linaloweza kudumu kama halina ibada ya kweli  hivyo kuabu ni kwa muhimu kwa uhai wa kanisa na mwandamu. Hata hivyo kwa kuwa kila binadamu ana mipaka namna tunavyoweza kumuabudu Mungu inategemeana sana na jinsi Mungu anavojifunua kwetu.

     Kuabudu ni njia ya neema kubwa sana ya msaada ulio juu sana wa mwanadamu, wana saikolojia wanakubali kuwa watu wengi wanaoishi bila kuabudu na wale wenye kuabudu wanatofauti kubwa sana ya kustahimili migandamizo ya masumbufu ya maisha “stress” kwamaana kuwa wanaoabudu hupunguza kwa kiwango kikubwa kuliko wasioabudu aidha tunapoabudu Roho Mtakatifu hutuunganisha na ndugu zetu na jamaa zetu katika Kristo katika ulimwengu wa roho kumuabudu Mungu mmoja aliyejifunua kwetu

    Somo hili basi ni la muhimu kwani litakuwa likikupa maelekezo  ni namna gani tunaweza kumuabudu Mungu na kuchukuliana na mzingira ya kumuabudu Mungu ikiwemo nafasi ya Muziki katika kuabudu na vionjo vingine mbalimbali katika kukamilisha swala zima la kuabudu fuatana nami basi Mchungaji Innocent Kamote katika uchambuzi wa somo hili Elimu kuhusu kuabudu Theology of wortship, Maombi yangu ni kuwa somo hili litakusaidia kukuweka karibu katika mahusiano yako na Mungu na wengine na ni maombi yangu pia kuwa utakapojifunza somo hili utakuwa ni msaada mkubwa sana kwa wengine na katika makanisa ya Mungu katika swala zima linalohusu kuabudu na kusababisha waweze kuwa na ukaribu sana na Baba yetu wa mbinguni kupitia kuabudu, Mungu akubariki

SURA YA KWANZA KUABUDU NI NINI
     Kwa kuwa kuabudu ni swala muhimu sana kwa katika maisha ya mkristo na uhai wa kanisa asili yake ni lazima ikaeleweka kwani kuna maelezo mengi sana kuhusu kuabudu, na kila iitwapo leo maelezo zaidi yanazidi kutolewa, lakini kupata Maelezo yenye kutosheleza kwa ukamilifu sio kitu rahisi, Hata ingawaje wengi wanaabudu na viongozi wa ibada wanaongoza kuabudu lakini hawajawahi kujaribu kuelezea kwa wazi kwa watu maana yake ni nini?
    Hakuna sababu za maana za kuelezea Kuhusu uzoefu wa kuabudu  ni ujuzi wa kiroho ni kuingia katika mawasiliano ya kiroho na Mungu aliye juu sana uhusiano huo kamwe hauwezi kuelezeka kwa maneno au kanuni za kawaida vyovyote iwavyo kuabudu kutakuwa na maana kama mwabudu atakuwa na ufahamu wa asili ya kuabudu

1.        MAANA YA KUABUDU.

     Kuabudu  maana yake hasa inatokana na  lile neno linalotokana na Kiingereza  Worship  linatokana na neno la zamani sana la kiingereza cha kizamani likisomeka kama Worthship au weorthscipe ambalo ni muunganao wa maneno mawili  worth na Ship na katika matumizi ndipo likaweko neno worship  ambalo maana yeke ni kustahiliisha au kukipa kitu uthamani, hivyo kuabudu ni kustahiliisha, au kutoa thamani, kutukuza,kuhimidi na hili linafanyika kumuelekea Mungu kwani yeye ni mfalme mkuu, ni Muumba wetu ni Baba  ni kila kitu Zaburi 95;1-7
        Mtakatifu Augustino alisema hivi “Thou hast made us, O God, and our hearts are restless until they find rest in Thee.” Kwamba ingawa umetuumba sisi ee Mungu mioyo yetu haipati utulivu mpaka tupate pumziko katika wewe. Kuabudu kwa kiibarania  kunaelezwa kupitia neno “Shahah” hii ni hali ya kujitoa  wewe mwenyewe  kwa Mungu kwa yale aliyoyafanya ,  Kwa kawaida Mwanadamu aliumbwa awe na uhusiano na Mungu kwa mfano wa Mungu hivyo iko kiu ndani ya Binadamu ya kuabudu lakini uhuru wa kuchagua  alionao mwanadamu ndio unaomuongoza kuchagua matendo maovu. Kuabudu ni kumtumikia Mungu ni kukubali yeye awe Bwana nasi watumwa wake Kutoka 3;11-12 kusudi kubwa la Mungu kutuokoa na kuwaokoa Israel ni ili wapete kumuabudu Matendo 7;6-7 kila mtu aliyeokolewa hawezi kuishi bila Ibada, Ibada ni njaa au kiu inayojitokeza ndani ya mwanadamu kujisikia kuwa na ushirika na Mungu, kiu hii au njaa hii hutimizwa pale tu tunapomfikia Mungu na tunapopata muda wa kuwa Naye.Katika uwepo wake kuna ukamilifu wa Furaha Zaburi 16;11 Kwa msingi huo basi kama katika Kanisa la Mungu hatusikii uwepo wake kuna uwezekano wa kuweko hitilafu katika kuabudu kwetu yaani  inatisha jinsi gani?

2.       MAANA YA KUABUDU KIBIBLIA

     Usomaji wa Biblia ni moja ya njia ya kupata picha itakayotuongezea ufahamu kuhusu kuabudu, Kuna  Maandiko mengi katika Biblia na maneno yanayotafasiriwa kama kuabudu, lakini maneno ya asili yahusuyo kuabudu  katika Biblia yanatupa mwanga zaidi na neno la Kiebrania Shahah  hutumika kuelezea mtazamo wa akili na mwili katika kuabudu ambako ni kujitoa kwa ukamilifu kwa Mungu Warumi 12;1. Kwa kiyunani tuna neno  Proskuneo ambalo maana yake ni kupiga busu kiss, kuibusu mikono, uso, au kuinama hata chini kwa paji la uso ambalo kwa maana nzuri ni kujitoa kikamilifu Martin Luther alisema “kuwa na Mungu ni kumuabudu yeye”
     Mungu alituumba  kwa kusudi la kumuabudu yeye Ufunuo 4;11 inaonyesha kuwa tuliumbwa kwa kusudi lake, Ni mapenzi ya Mungu kutaka kuwasiliana na kila mmoja na kujifunua kwake Biblia inaonyesha kuwa alijifunua kwa namna nyingi Warumi 1;20,Ufunuo 4;11,2Timotheo 2;3-16, Warumi 8;16,Yohana 1;17-18 Mungu anataka kabisa tumuabudu yeye na anahitaji mwitikio wa kila mmoja ni sehemu hiyo basi ya mwitikio wa Mwanadamu ndio unaopelekea kuhimidi, kutukuza, kushukuru, kuadhimisha, n.k. Mtu anapomuomba Mungu au kupeleka malalamiko yake kwa Mungu anawasiliana na Mungu lakini sio ibada ya kweli Mungu anatafuta watu watakaomuabudu katika Roho na kweli Yohana 4;23-24.
SURA YA PILI UMUHIMU WA KUABUDU
     Kama kuna jambo la Muhimu sana duniani ambalo mwanadamu na kanisa wanaweza kulifanya basi ni kuabudu amini usiamini Kama kuna jambo la muhimu ambalo ni la muhimu mkristo anaweza kulifanya basi ni kumuinua Mungu juu yaani kumuabudu kama alivyowahi kusema askofu mkuu William Temple, wa kanisa la Presbeterians, “Kumuabudu Mungu, kumsifu, kumuhimidi, kumwadhimisha  ndio njia ya juu kabisa ya mkristo ya uhusiano kwa Mungu” lakini kuabudu pia ni zaidi ya swala hilo kwani kuna faida nyingi zipatikanazo kupitia kuabudu Faida hizo ni zipi hapa ziko kadhaa 

*      Kuabudu kunaimarisha umoja wetu na Mungu

     Kwa kawaida mwanadamu anapokuwa mbali na Mungu anakuwa mpweke na mnyonge  na anakuwa hana furaha, kuasi kwake kunaleta hatia  na misiba moyoni  na anakuwa hana amani ya kweli  na kwa hivyo anakuwa na kiu ya kuungana na Mungu na wanapotaka kufanya vizuri wanashindwa (Warumi 7;19) Njia pekee ya kumsaidia mwanadamu kutoka katika hali  hizo ni kuabudu, kwa kadiri mtu anavyomkaribia Mungu  ndivyo unavyojiona kuwa hufai na unajielewa kuwa jinsi usivyomtii na kuwa mbali naye na kwa kuwa hupendi kuwa mbali naye  unatubu anakusamehe  na unapata amani Isaya 6;1-8 Kutengwa na Mungu ni adhabu kubwa sana kuliko zote duniani Mwanzo 4;12-14.na tatizo kubwa tulilo nalo ni kuwa watu wengi hawana uhusiano mzuri na Mungu.

*      Kuabudu kunakamilisha hitaji la kushirikiana na wengine.

     Kama mwanadamu alivyo na kiu ya kuwa na ushirika na Mungu hali kadhalika ndivyo pia anavyihitaji  ushirika na wengine , mwanadamu aliumbwa  kwa ajili ya ushirika na wengine “Human Being is a Social being” Mwanzo 2;18 hivyo kuna hali ya kuwahitaji wengine  na kuwa sehemu ya kundi  hitaji hili linaweza kutimizwa kwa ibada za pamoja katika Kanisa , familia,majirani, kukutana pamoja kushirikiana, kutiana moyo kuomba na kusifu pamoja ,kusikiliza mahubiri na kuombeana Wakolosai 3;16-17,WEaefeso 5;19-21

*      Kuabudu kunatoa maana ya maisha na kusudi la kuishi.

    Maisha hayana maana kama hatujui kwa nini tunaishi, Mwanadamu siku zote ana hamu ya kujua yeye ni nani? asili yake ni wapi? Ametoka wapi?na hatima yake ni nini?nani ameniumba n.k. Zaburi 8;3-9, Tunapomuabudu Mungu ndipo ukweli kuhusu maana na kusudi la  la sisi kuishi  linatiririka, sisi tu watu wake na kondoo za malisho yake yeye ni Mchungaji  wetu, na kuwa ni Bwana tunapaswa kumtumikia Mungu  na kuwa siku moja tutakuwa naye kweli hizi zote zimejificha katika kuabudu

*      Kuabudu kunatusaidia kutambua mipaka Yetu.

    Kuabudu kunamfanya mwanadamu kutambua mipaka yake, mwanadamu anapomuabudu mwenyezi Mungu wa milele  anapata kujitambua jinsi alivyo dhaifu, na kuwa ni wa Mudamfupi tu hapa duniani, na kuwa anamuhitaji Mungu na kuwa Bila msaada wa Mungu hatuwezi na kuwa bila yeye hatuishi Mathayo 4;3-4, Hivyo hatuwezi kujitegemea bali tunamtegemea Yeye hili tunaweza kulitambua kupitia kuabudu

*      Kuabudu kunatusaidia kupata majibu ya matatizo yetu katika maisha

    Maisha yana matatizo mengi sana na ni wachache tu wana weza kuyaepuka, Magonjwa, hali za kukata tama, mishituko, kuudhiwa, huzuni, hatia ya dhambi, uovu, Migandamizo na misongo ya mawazo n.k. hii ni mizigo ya kawaida katika maisha Yesu alitoa mwaliko kuwa njooni kwangu ninyi nyote wenye kulemewa na mizigo nami nitawapumzisha Mathayo 11;28 ni kwa kuabudu tu  tunaweza kuona tunapata faraja na kutiwa nguvu, wengi wanaokwenda ibadani na mizigo wanatoka wakiwa wepesi na wenye amani na Furaha Muujiza wa kumuabudu unachukua nafasi 1Samuel 1;6-20, Isaya 40;28-31 Kuna majibu ya maisha katika kuabudu hali ngumu zinazo tuzunguka  na matatizo tuliyonayo yanaweza kupata ufumbuzi kupitia kuabudu 1Samuel 30;1-18.

*      Kuabudu kunatupa nguvu za kuangusha ngome na vifungo vya adui.

     Shetani ni adui yetu mkuu na siku zote anatafuta kutushambulia huku akituzingira kwa namna mbalimbali na kwa ngome nzito siri kuu ya ngome zake na mashambulizi yake kushindwa ni kuabudu Matendo 4;14-31, Matendo 16;19-31.

*      Kuabudu Kunatupa nafasi ya kupokea maelekezo au wito kwa utumishi.

     Matendo 13;1-3 Ibadani ndipo mahali ambapo mwanadamu anaweza kupokea maelekezo mbalimbali na nguvu za wito kwa utumishi, hapa tunakuwa na nafasi ya kupata maelekezo kutoka kwa Mungu kupitia Roho wake Mtakatifu, kuzungumza na mioyo yetu au akili zetu au kupitia mahubiri ya Neno la Mungu, unabii, nyimbo, maombi n.k hapo ndipo hali za kumuinua Mungu hujitokeza na kiu ya kumtumikia inahuishwa
SURA YA TATU MISINGI YA KUABUDU
     Kuabudu kwa kweli lazima kuwe na misingi, misingi hii ni sifa za kuabudu Kikristo ili ibainike kuwa tunamuabudu nani ni muhimu basi kujifunza Misingi hii 

1.       Kuabudu kwa haki Lazima kumlenge Mungu

     Hapa jambo la msingi kwanza halijengwi ni namna gani tunaabudu lakini nani tunamuabudu ni swali la msingi sana hata kabla ya kuangalia ni namna gani tunaabudu ni lazima tujiulize nani tunamwabudu? Wote tutakubaliana nami kuwa katika kila jamii kuna nguvu ambayo inaaminika kuwa iko juu ya mwanadamu na ina nguvu, hekima na uweza kuliko tulivyo wanadamu na nguvu hii ina majina tofauti tofauti nguvu hii huitwa Mungu, Mungu huyu amejifunua kwa wanadamu kwa njia nyingi na kwa namna tofauti Lakini Biblia pekee ndio kitabu kilicho kitakatifu kuliko vyote na kinamfunua Mungu kwa viwango halisi vyenye kutosheleza kiu ya mwanadamu ya kuabudu na kupata thawabu kutoka kwa Mungu
     Katika Zaburi 19;1-2 Tunaona Mungu akijifunua ukuu wake katika nguvu kubwa ya asili kama Radi na mtiririko mzima wa kupambazuka kwa jua na machweo ya jua
     Katika Zaburi 119;130 tunaona kwamba Mungu ame zungumza na wanadamu  kupitia Neno lake kwa njia rahisi
Mungu pia anazungumza moja kwa moja  kupitia mioyo yetu , katika Yohana 6;44 Yesu alisema  mtu hawezi kuja kwangu asipokuwa amevutwa na Baba sauti hii yenye kuvuta ni sauti ya moyoni kwa njia nyingine ndiye anayetufanya tuwe na ujuzi kumuhusu, tunahisi nguvu zake, upendo wake na kwa msingi huo ibada ya kweli huchochewa na Mungu mwenyewe ndani yetu kupitia Roho wake Mtakatifu kwa hiyo kile ambacho Mungu hukifunua katika mioyo yetu hukubaliana na kile alichokifunua mwenyewe katika Biblia, katika uumbaji na katika Maisha ya Yesu Kristo,Mungu hujifunua kama

a.       Ni Muumba wetu – Anastahili heshima na adhama Zaburi 139-15,8;3-4 ni kimbilio letu na usalama wetu kwa hivyo tunapaswa kumtegemea.
b.      Ni wa kutumainiwa Zaburi 46
c.       Ni Mfalme wetu wa haki kwa hiyo anastahili kusifiwa Zaburi ya 47
d.      Ni baba yetu wa Mbinguni kwa hiyo anastahili upendo wetu na utii wetu Mathayo 6;32-33
     Kwa msingi huo basi kila kurasa katika Biblia zinatuonyesha ubora wa Mungu kwetu jinsi alivyo mkuu, Kumuabudu pekee ndio muitikio wetu kwa kadiri anavyojifunua kwetu, Mitazamo yetu na tabia zetu tunazipata kutoka kwake Yeye hutamani pendo lake limiminike ndani yetu na ya kuwa tumuabudu ndio maana Yohana anasema tunampenda kwa sababu alitupenda kwanza 1Yohana 4;19 na Zaburi ya 145 inafunua jinsi Mungu alivyo kwa maneno haya yafuatayo;-
Ni mwenye kujali
Ni wa Rehema
Anataka kutusaidia
Anataka tuwe na furaha
Anaweza kukutana na mahitaji yetu yote
Yuko wakati wote
Anasamehe
Ni mwema kwetu
Anapatikana wakati wote
Ni wa haki
Baada ya kujifunza jinsi Mungu alivyo mwema na anavyo tujali mwandishi wa zaburi ya 8 anahoji upendo wa Mungu kwa mwanadamu kwa kusema Mwanadamu ni nani hata umkumbuke? Na mwana wa Binadamu hata umwangalie sasa ni muhimu kuona kuwa wale wanaomuheshimu na kumuabudu wana ahueni tofauti na wale wasiomuabudu na kumuheshimu wao wanaitwa wapumbavu kwa sababu hawana kimbilio wala msaada wakati wa mateso Zaburi 46;1-3, lakini wale wasioamini katika Mungu huitwa wapumbavu Zaburi 53;1-3.

YEYE ASIYEMFUATA MUNGU
YEYE ANAYE MFUATA MUNGU
Hana amani Isaya 57;20-21

Amebarikiwa kwa amani Warumi 5;1
Amepungukiwa na ufahamu wa kweli Matendo 28;26-27
Ana uhakika wa Sauti ya Mungu Yohana 10;2-5

Amedanganyika Yeremia 17;9
Anajulikana kwa uaminifu kwa Mungu 2Koritho 1;12 Kolosai 3;9-10

Amejaa dhambi Efeso 2;1
Huru mbali na dhambi 1Yohana 1;9,Yakobo 3;17-18

Anangojewa na kifo cha milele Efeso 2;1
Anatunukiwa uzima wa milele Yohana 3; 36


2.       Kuabudu ni lazima kuwe katika Roho na kweli Yohana 4;23-24 “Spiritual”

     Tunapozungumzia kuabudu katika Roho na kweli maana yake kuu hasa ni kwamba lazima kuabudu kwetu kwanza kutokee ndani sana ya moyo, Ibada ni swala la moyo na ufahamu, pia katika uwepo na upako wa Roho Mtakatifu Kwa kuwa Roho wa Mungu anaishi ndani yetu Yohana 14;16-17 Roho hutenda kazi katika ibada hivyo ni muhimu akahusika akaachiwa atuelekeze namna tunavyoweza kubudu.
     Katika kweli ni nini? Ni neno la Mungu Yohana 17;17 , Mathayo 26;27-30, Pia Kristo ndiye kweli Yohana 14;6 hivyo ibada ya kweli lazima ifanyike sawa na Neno la Mungu kupitia Yesu Kristo au sawa na injili ya Yesu Kristo Marko 7;6-7

3.       Kuabudu ni Lazima kuanze  na mtu Binafsi “Personal”

     Msingi mwingine wa Ibada ya kweli ya Kikristo ni kwa mtu moja mmoja Binafsi, uhusiano wa Mungu kwa mwanadamu hauanzi na mkumbo au kundi la watu bali na mtu mmoja mmoja Binafsi anakuwa na uhusiano na Mungu “It is a direct Personal Encounter” Mwanzo 12;7,8, 5;24, Nehemia 1;1-10, Hata hivyo ingawa kuabudu ni swala Binafsi  hii haina maana kuwa hatupaswi kushirikiana na wengine katika ibada Mithali 18;1

4.       Kuabudu ni lazima kuwe kwa ushirikiano Waebrania 10;25 “ Corporate”

     Msingi wa kuabudu hautoshi tu kuwa kwa mtu mmoja mmoja binafsi  lakini pia kwa ushirikiano, uhusiano Binafsi na  Mungu katika kusamehewa dhambi hili ni jambo la kwanza  ambalo ndilo linalotuunganisha katika mwili wa Kristo Warumi 12;5, 1Koritho 12;12-13 hivyo ingawa kuabudu  binafsi ni muhimu lakini kuabudu pamoja nako ni  kwa muhimu zaidi

5.       Kuabudu ni lazima kuwe kwa kumaanisha “sincere”

     Kwa kuwa ibada ya Kikristo inahusu mtu na watu  ni rahisi kufanya ibada kwa kusudi la kuwapendezesha watu, kwa kuwa wana macho na masikio  na hivyo kunaweza kutolewa maombi, shuhuda, Nyimbo na neno ambalo msingi wake  ni kuwapendeza watu, Ibada ya jinsi hii sio ibada ya kumaanisha au makini  ibada za jinsi hii kwa mujibu wa mafundisho ya Yesu zitakupatia thawabu yako kutoka kwa watu hapa hapa  Duniani Lakini mbinguni ukawa umekataliwa Jambo lolote lile linalofanywa katika ibada kwa kusudi la kuwapendezesha watu halina thawabu mbinguni Mathayo 6;16-18,6;1-4,5-8 Ibada ni lazima ilenge kupelekwa kwa Mungu neno Sincere maana yake pasipo kuigiza, ya kweli na ya uaminifu hizi ndizo ibada zinazo mpendeza Mungu

6.       Kuabudu ni lazima kuwe kwa unyenyekevu “Humble” 

    Ibada ya kweli ya Kikristo ni lazima ijengwe au ifanyike katika msingi wa unyenyekevu, kwenda mbele za Mungu huku tuna kiburi au tunajihesabia haki au tusio na moyo wa unyenyekevu kutaifanya ibada yetu  kuwa ibada isiyo na faida Luka 18;9-14 Unapokwenda ibadani ubnapata Nafasi ya kujiona kama vile Mungu anavyokuona  hivyo utajiona jinsi ulivyo na mapungufu na utakuwa mnyenyekevu Kumbuka Mungu anasema katika Isaya 57;15 Kuwa Mungu hukaa na mtu mwenye kupondeka au mnyenyekevu aliyetubu,Isaya 66;2 anayetetemeka.

7.       Kuabudu ni lazima kuwe kwa uhuru “Free & Spontaneous”

     Uhuru huu hauna maana kuwa mtu anajifanya vyovyote atakavyo bila kufuata mpango, Lazima kuwe na utaratibu, Lakini usiwe utaratibu chuma Bali utaratibu ambao utaruhusu Roho kutupeleka atakako ikiwa ni pamoja na hisia zetu kama zilivyo 2Samuel 12-16,1Nyakati 15; 1-29, Kuna wakati ambapo mtu anaweza kuabudu na kuchukuliwa katika uwepo wa Mungu kiasi cha kushangaza lakini hata katika hali hiyo mtu hatakiwi kuingiliwa anatakiwa kuachiwa huru 

8.       Kuabudu lazima kuambatane na kuishi

     Kuabudu kwa mkristo ni lazima kuambatane na kuishi sawa na Mungu anavyotaka, Ibada haiwezi kukubalika kama hatuishi sawa na Neno Amosi 5; 21-24, ili ibada zetu zikubalike hatuna budi kuishi au sawa na neno la Mungu ndipo tutapata kibali Mathayo 5;23-24 si kila mtu asemaye Bwana Bwana atakayeingia katika ufalme wa Mungu Bali kwa kuishi au kutenda  Mathayo 7;21 Hivyo jambo lolote au yoyote tufanyayo tuyafanye kwa utukufu wa Mungu.

9.       Kuabudu ni lazima kuwe kwa gharama.

     Ni muhimu kufahamu kuwa kuabudu ni gharama na Baraka za kweli za kiroho hazipatikani kirahisi hivi hivi, wakati mwingine kuabudu kutatupelekea kugharimika kwa maisha yetu, mali zetu au watoto wetu, Nyakati za agano la kale ili kumuabudu Mungu watu walihusisha ibada zao na utoaji mkuu wa vitu vilivyonona yaani wanyama na dhabihu Mwanzo 4;3-4, hakuna ibada inayoweza kukubalika na Mungu isiyo na gharama, Kaini alileta sehemu zilizonona na Mungu akakubali ibada yake, Nuhu aliposhuka salama kutoka katika safina iliyookoa maisha yake na wanawe alimtolea bwana ibada ya thamani Mwanzo 9;18-22, Angalia maisha ya Ibrahimu tangu alipoitwa na Mungu alikuwa Muabudu aliyejenga madhabahu kila wakati na juu ya madhabahu hiyo alitoa kitu cha thamani dhabihu Mwanzo 12;8,15;1-21. Daudi mfalme mkuu sana katika Israel alikuwa muabudu Mungu aliyehakikisha anamuabudu Mungu kwa kila kitu chenya thamani 1Nyakati 11;15-19, 2Samuel23;15-17 alimtolea Mungu maji ya thamani sana yaliyogharimu maisha ya watu, alikataa kupewa kiwanja Bure kwaajili ya kujenga nyumba ya kuabudia 2Samuel 24;24 “Wala sitamtolea BWANA, Mungu wangu sadaka za kuteketezwa nisizozigharimia.” Kama tunataka kuona ibada zenye Baraka ni muhimu kwetu tukakubali kugharimika kwaajili ya ibada hizo, Kujitoa, kuombea na kumpa Mungu vitu vya thamani vya hali ya juu ili Baraka za Kiroho na za kimwili ziweze kuwa pamoja nasi.
SURA YA NNE MATOKEO YA KUABUDU
     Tunaishi katika ulimwengu ambao umejaa matatizo mengi, vita, mafarakano, n.k na kadiri tunavyoendelea kuweko hapa ulimwenguni ndivyo wakati mwingine tunavyochanganyikiwa zaidi na wakati mwingine tunaweza hata kupoteza malengo yetu katika maisha kwa nini kwa sababu ulimwengu pasipo Mungu  unakuwa ulimwengu wa kisanii usio na faraja na ulimwengu huu tulio nao wanaoishi ndani yake hawajali kitu kuhusu Mungu wala hawampendi wala hawana hamu kuhusu mambo ya Mungu, ili ndoto zetu katika maisha ziweze kutimia Basi njia ya kuabudu ni ya muhimu sana katika maisha ya mwanadamu hili ndilo hitaji kubwa zaidi la mwanadamu

Tunapoabudu wazo kuhusu Mungu hujengeka

     Kadiri watu wanavyoabudu ndivyo wazo kuhusu Mungu linajengeka, Mungu anatukumbusha kuhusu pendo lake kwetu, utakatifu wake, na nguvu, tunakumbuka ukuu wake na kuona kuwa kumbe anaweza kukaribiwa, hatujisiikii upweke, tunakuwa na matumaini kwa sababu ana nguvu za kutosha kukutana na mahitaji yetu, hofu zetu zinakuwa kama ujinga tu kwa sababu anatupenda na anatujali tunaanza kujitambua kuwa sisi ni watoto wake na raia wa Mbinguni na kuwa Mungu ndiye mfalme wetu, Mungu huyaona mapito yetu kama njia ya kujifunza na kukomaa anaziona huzuni zetu kama njia ya kumtafuta yeye, anayaona magonjwa yetu kama njia ya kuonyesha pendo lake kwetu tunarejezwa katika uhalisia kuwa Mungu ni pendo na kuwa anatuelewa na ni masaada ulio karibu
     Kuabudu sio jambo la kupuuuzia hata kidogo ni jambo lenye manufaa na lenye kuleta mtiririko thabiti Biblia imejaa mifano mingi sana kuhusu kuabudu na matokeo ya kuabudu swala hili limeleta matokeo makubwa kwa watu binafsi na kwa kanisa kuabudu sio kupoteza muda ni lazima watu wajijengee mazingira ya kupenda kuabudu
·         Muhubiri maarufu Duniani John Wesley alipenda sana kuabudu na alipata mafanikio makubwa sana na kwa sababu hiyo yeye na  familia yao walipata mafanikio makubwa kaka yake Charles Weslay ni moja ya watunzi wa nyimbo nyingi sana katika tenzi za Rohoni na mama yao aliwafundisha kuimba na kumuabudu Mungu
·         Muhubiri maarufu duniani Benny Hinny  hufanya maombezi na huduma yake huambatana na miujiza mikubwa kwani hafanyi maombezi bila kuabudu hupenda sana kuabudu
·         Muhubiri Wilifred Lay wa Mombasa nchini Kenya miaka ya nyuma alikuwa na washirika 20,000 waliokuwa wakiabudu pamoja katika mji huu amabao ni mji wa kiislamu amefanikiwa kwa sababu ya  kuwa na ibada nzuri za kusifu na kuabudu kila jumapili jioni  na alilipa jina kanisa lake Jesus cerebration center JCC
·         Miaka mingi nyuma huko Ufilipino watu waliabudu na kufunga na kuomba kwa kusudi la kutafuta  uso wa Mungu moto mkubwa uliwaka juu ya kanisa lao na watu wengi wakajua kuwa labda kanisa linaungua kumbe Roho wa Mungu alikuwa ameshuka na watu wengi waliokolewa wakiwemo askari wa zima moto waliofikiri kuja kuzima moto
·         Nyakati za kanisa la kwanza watu walimuabudu Mungu na kumuadhimisha na matokeo yake pale mahali pakatikiswa nguvu za Mungu na Roho zikashuka,Matendo 4;23-31,16;25-28
·         Elisha nabii alipata ufunuo wa neno la Bwana wakati fulani baada ya kuwa na muda wa kuimba kwa kinanda  2Wafalme 3;11-20 ,miujiza ya maji na ushindi wa vita ulikuja baada ya watu hawa kuabudu
·         Wana wa Israel walimsifu Mungu na kutii maagizo yake ya kuuzunguka ukuta wa mji ngome ya Yeriko  na ukuta ukaanguka kwa kuzama Yoshua 6;15-16,20-26
·         Wakati wa kuweka wakfu hekalu ibada ilimpendeza Mungu na utukufu wa Mungu ulishuka  kwa sababu watu walifanya ibada ya kipekee sana 2Nyakati 5;7-14 kuabudu kuna matokeo makubwa sana  katika maeneo mbalimbali ya maisha yetu kamwe hatupaswi kupuuzia kuabudu
·         Paulo na silla walifanya ibada gerezani na malango ya gereza yakafunguka pamoja na vifungo vyake
·         Kuabudu kunaleta ushindi katika maisha na mitazamo tofauti wakati waisrael wakimuangalia Goliath na kuliona ni jitu kubwa na kuwa litawapiga wakaogopa Daudi ambaye ni muabudu Mungu alikuwa na matazamo tofauti Yeye aliona kuwa Goliathi ni mkubwa kiasi ambacho akimpiga kwa kutumia kombeo hatamkosa!
·         Kutoka 33;7-22 na 34;1-5, Mungu alimuahidi Musa kuwa angeuona utukufu wake hii ilikuwa ni nafasi ya kipekee kwani alikuwa Muabudu  , Mungu alijenga uhusiano na Musa kama wa mtu na rafiki yake aliongea na Mungu uso kwa uso, kuabudu kunatufanya kuwa rafiki wa Mungu
SURA YA TANO KUABUDU PAMOJA NA WENGINE.  (THE CONGREGATION AT WORSHIP)
     Moja ya mambo yanayo mpendeza Mungu ni pamoja na watu wake kumuabudu pamoja kwa kujitoa kwa pamoja, kumuhimidi na kumuomba na kumsifu katika ushirika Jambo hili linampendeza Mungu upeo , lakini je kila kusanyiko linaweza kukubalika na Mungu ? je ni wapi tunaweza kukusanyika na kuabudu pamoja na ni kwa namna gani na kwa utaratibu gani? Je namna tunavyoabudu leo chimbuko lake ni wapi tunapo jaribu kujibu maswali haya ndipo tunapoweza kupata nafasi ya kuonyesha umuhimu wa kuabudu pamoja na maana yake 

Mwanzo wa kuabudu pamoja

     Namna tunavyoabudu pamoja leo ni matokeo ya mchanganyiko wa namna nyingi, lakini msingi imara na mzuri wa kuabudu pamoja kibiblia unatoka kwa wayahudi na nyakati za kanisa la kwanza namna na jinsi walivyoabudu ndiyo namna na jinsi tuwezavyo kuabudu

Chanzo kutoka kwa wayahudi

     Kuabudu kwetu kama wakristo msingi wake umetokana na msingi wa ndani sana wa ibada za kiebrania. Marabi au waalimu na wanafunzi wao waliabudu hekaluni katika hekalu ambalo Herode alilijenga na katika masinagogi, Yesu mwenyewe ilikuwa desturi yake kuabudu katika masinagogi wakati wa sabato Luka 4;16, mpaka mwaka wa 70 B.K wakati hekalu lilipobomolewa ndipo wakristo walipoacha kuabudu hekaluni, na hata ingawaje baada ya hekalu kubomolewa na pamoja na ufa kati ya wakristo na wayahudi kuzidi kujitokeza wafuasi wa Yesu waliendelea kuabudu katika masinagogi na kumbuka kuwa hata injili ilipokuwa inahubiriwa mara nyingi Kina Paulo walianza kuhubiri kwa jamii ya wayahudi katika masinagogi kabla ya kuanza kuwahubiri wapagani walifanya hivyo katika masinagogi yote chini ya utawala wa kirumi na hata ilipokuja kutokea utengano wa moja kwa moja kati ya imani ya kiyahudi na ukristo , wakristo waliondoka na vimelea vya ibada za kiebrania.
     Ingawa kuabudu katika Hekalu hakukuwa na nyongeza yoyote katika imani ya ukristo kwa sababu moja ya mambo muhimu ya hekaluni ni pamoja na sadaka za kuteketezwa za namna mbalimbali athari za ibada za kiebrania ziliendelea kuonekana katika ukristo ikiwemo utoaji wa sadaka lakini sio za wanyama  na matumizi ya zaburi kama njia ya kumsifu Mungu, Zaburi ziliimbwa, zilikaririwa na kurudiwarudiwa kama nyimbo rahisi hali hii iliambukizwa katika imani ya ukristo na ibada zake ingawaje mfumo ulikuwa zaidi wa katika masinagogi kuliko hekaluni.
    Mfumo wa kiibada katika kiibrania pia ulibadilika baada ya kuvunjwa kwa hekalu na kwenda utwanyikoni ambapo huko masinagogi yalijengwa na kusomwa kwa sheria na manabii ukawa ndio msingi mkuu wa ibada za kiebrania kwani maswala ya sadaka za kuteketezwa na sanduku la agano hayakuweza kufanyika tena lakini kabati la kutunzia magombo ya chuo katika sinagogi yamekuwa kama aina mpya ya sanduku la agano, Ibada katika masinagogi zilikuwa rahisi sana kuliko za hekaluni hakukuhitajika tena mfumo wa makuhani na mkuu wa sinagogi alishirikiana ibada na watu wengine katika jamii yao, Pamoja na kusoma maandiko , kusifu, kuomba na kumtukuza Mungu kuliendelezwa, watu wote walijihusisha katika kusifu, kuomba na kukariri amri kumi na “shema”  kumbukumbu la Torati 6;4-5 “Sikia, Ee Israeli: BWANA Mungu wako, ni BWANA mmoja. Mpende BWANA Mungu wako kwa moyo wako wote na kwa roho yako yote na kwa nguvu zako zote. Amri hizi ninazokupa leo zitakuwa katika moyo wako. Wafundishe watoto wako kwa bidii. Nena kuhusu amri hizi uketipo nyumbani na wakati utembeapo njiani, ulalapo na uamkapo. Zifunge kama alama juu ya mkono wako, zifunge juu ya paji la uso wako. Ziandike kwenye miimo ya milango ya nyumba yako na juu ya malango yako ukiri huu huitwa shema kiibrania ulikuwa ni kama tangazo la imani na watu waliitikia Amin kama ishara ya muitikio.

Chanzo kutoka kwa mitume

    Nyakati za kanisa la kwanza wakristo nao waliendeleza mfumo wao wa kuabudu mfumo huu ulifanana na ule ulioendeshwa katika masinagogi ya wayahudi kulikuwa na usomwaji wa maandiko kwa kawaida ilikuwa maandiko ya manabii na mitume, kulikuwa na kutukuza, kusifu na maombi pamoja na sadaka lakini zaidi ya hayo kulikuwa na swala la meza ya bwana au kuumega mkate na swala la ubatizo, hii ni sawa na Matendo 2;42-47 hii ndio hasa ibada kamili ya agano jipya iliyokuwa ikifanyika wakati wa mitume, Maswala kama haya yalifanyika lakini ilikuwa jumapili kwa ajili ya kukumbuka siku bwana alipofufuka, Ibada zilikuwa rahisi na isiyo na mfumo maalumu Roho wa Mungu alipewa nafasi kubwa kuingilia kati mfumo wa ibada si kila wakati.

Umuhimu wa kuwa na mapangilio katika ibada za pamoja
     Pamoja na kuwa historia inaonyesha kuwa nyakati za kanisa la kwanza ibada hazikuwa na mfumo maalumu lakini hii sio kibali cha kutokuwa na mpangilio katika ibada, mpangilio katika ibada ni jambo la Muhimu kwani Mungu sio Mungu wa machafuko bali ni Mungu wa utaratibu, kupangilia ibada kutaweza kuleta msaada mkubwa kwa wale wanaohusika katika kuabudu, sasa ibada inaweza kupangiliwa vipi kwani kuna maandiko ya kusomwa, maombi, muziki, nyimbo vyombo, mahubiri, sasa basi kipi kianze na kipi kimalizie kwa ujumla hakuna mfumo maalumu katika ibada kuwa nini kianze na nini kimalizie lakini kuna vimelea  fulani vya namna ya kuabudu ambavyo vimekusanywa kitaalamu vimelea hivyo ni kama ifuatavyo

*      Utambuzi
Moja ya jambo muhimu sana katika ibada ambalo ni la msingi lakini gumu kidogo kulielezea ni kutambua kile unachokiabudu, makanisa mengi huwa na tabia ya kujisahau na kuanza moja kwa moja na nyimbo  bila kwanza kuweka mazingira yanayomfanya mtu kutambua kuwa anamwabudu nani kwa hivyo kunaweza kuwako wimbo au maneno yanayowakumbusha washiriki katika ibada kuwa wamekuja kumuabudu Mungu.

*      Kusifu
Baada ya kuwa watu wametoa nafasi ya kutambua kuwa yuko Mungu basi wanapaswa kufurahia uwepo wake kwa msingi huo watakuwa na muda wa kusifu kwa nyimbo na muziki au watu wanaweza kusifu kwa kutumia maombi

*      Toba au kujitakasa
Baada ya kuwa watu wamemsifu Mungu kwa kutambua uwepo wake bado ni muhimu watu wakatambua kuwa Mungu huyo ni mtakatifu na kuwa tunapaswa kuziungama dhambi zetu kwa hiyo kunaweza kuwako nafasi ya ukimya ambapo washiriki wanapata nafasi ya kutubu dhambi zao wana weza kutumia nyimbo au maombi binafsi au sala maalumu kama baba yetu n.k

*      Utayari wa kupokea kutoka kwa bwana
Hii ni hali ya kukaa kimya kwa muda ili yamkini watu waweze kusikia kutoka kwa Mungu kwa kupata mwanga maalumu illumination ili kujua Bwana anataka nini kwao wanaweza kuangaziwa au kupata neema na kusikia kutoka kwa Bwana kupitia Neno la Mungu au Roho Mtakatifu

*      Kujitoa
Baada ya kuwa watu wamesikia kutoka kwa Bwana basi ni muhimu kwao kukubali kukutana na Mungu na kujitoa kwake kwa akili zake na nguvu zake  na moyo wake wote  hili linaweza pia kufanyika wakati wa maombi baada ya watu kulisikia Neno la Mungu hili ni jambo la muhimu

Kanuni za kupanga maswala ya ibada
    Mpangilio kuhusu ibada una kanuni zake za msingi na uandaaji mzuri na mpangilio mzuri wa ibada unaonyesha ubora wa mpangilio huo, tunapo zipangilia ibada zetu kwa mantiki nzuri. Mambo ya msingi ya kuzingatia katika upangaji wa ibada ili ilete matokeo yanayokusudiwa ni pamoja na 

*      Umoja.
Moja ya ubora wa kupangilia maswala ya ibada ni kuleta umoja  ibada ni lazima ionekane kuwa ni moja hii haina maaana kuwa ndani ya ibada hakuna vitu vingine vipo vitu vingi vinavyounda ibada  lakini lazima ionekane kuwa inategemeana hususani katika kiini chake ambacho ni kumuabudu Mungu kwa ujumla, kusudi la kumuabudu Mungu ni kuwako amani, kumshukuru na kupokea neema yake kusudi moja la kuabudu ni kumuabudu Mungu katika Roho na kweli vyovyote vile ibada itakavyokuwa lengo liwe kuleta umoja katika kumuabudu Mungu na mfumo wake

*      Utaratibu.
Jambo lingine la Muhimu katika ibada ni utaratibu, ingawaje umoja unasaidia kuifanya ibada yote kuwa kamili katika Lengo moja kusudi lilelile la kuifanya ibada iwe moja litaleta utaratibu “order within the service” Mungu ni Mungu wa utaratibu na hivyo lazima ibada iwe na uataratibu

*      Uwiano
Ili ibada izidi kuwa na umuhimu katika taratibu lazima uweko uwiano wa kila shughuli ndani ya mtiririko wa Ibada, Lazima utoe uwianao wa Muda unaolingana kulingana na uzito wa kila uanchotaka kifanyike yaani kama ibada ni ya dakika 60 basi ingawaje kila sehemu inayokamilisha ibada ipewe muda unaolingana yaani tunazungumzia swala zima la kusifu, maombi, kusoma neno, mahubiri n.k Mchungaji anatoa muda husika wa mahubiri yake kisha anahakikisha kuwa sehemu zinazobaki zinapewa uwiano sawa wa mwenendo mzima wa ibada kwa msingi huo ibada itakuwa inakwisha pia kwa wakati uliokusudiwa na kanisa la mahali pamoja

*      Mwenendo
Ibada haiwezi kuwa boara kama haina mwenendo ulio na mpangilio hii ni hali halisi ya mwenendo mzima wa ibada inatoka wapi na inakwenda wapi hili linaweza kusimamiwa vema kama anakuweko kiongozi wa ibada mwenye kutoa maelekezo kipi kinafuata ibada ambayo imesukwa vema kuanzia kuwaalika watu kuabudu mpaka mwaliko wa mwisho mara nyingi sana inaonyesha mwenendo makanisa mengine unaweza kuingia kuabudu usijue unatoka wapi na unakwenda wapi jambo kama hili si jema
*      Kilele.
Kufikia kilele ni moja ya maeneo muhimu sana ya maeneo ibada, na kwakuwa inaeleweka wazi kuwa ujumbe wa neno ndio sauti ya Mungu kuzungumza na watu wake kupitia mchungaji, kilele cha mahubiri ni lazima kiwe kilele cha ibada pia  ingawaje katika makanisa mengine mwaliko wa watu kuja kuliitikia Neno la Mungu ndio huhesabika kama kilele cha ibada watu wanapoitikia ile kweli ya neno walilolisikia kwa maana hii basi si vema kuweka neno kwanza kabla ya mengineyo au tunaweza kusema ni muhimu katika mpangilio wako Neno likawa mwishoni.
*      Vichocheo tofauti
Ni muhimu kwa makanisa ambayo hawapendelei mfumo fulani wa ibada kuwa na tabia ya kubadilibadili aina za ibada kila wakati kwani ukiisha kuwa na mfumo fulani mmoja wa ibada sasa unakuwa umejiundia utaratibu ambao ndio unaitwa “liturgy”liturujia ambalo maana yake ni utaratibu wa ibada kama mtu anachukizwa na utaratibu wa ibada nikiwa na maana kuwa haitaji liturujia basi anapaswa kuwa na vichocheo au vionjo tofauti tofauti visivyozoeleka katika kila mfumo wa ibada ,nyakati za kanisa la kwanza hakukua na mfumo maalumu wa ibada  lakini tatizo la jambo hili ni kuwa kutakuwa hakuna Muda maalumu wa kutoka katika ibada  ama itawapasa viongozi wa ibada kuwa na Muda wa kutengeneza muundo na mfumo wa ibada ya kila jumapili ijayo ili kuweko tafauti
Ushauri unaoweza kusaidia kuzifanya ibada za pamoja kuwa na maana zaidi
1.       Fanya maandalizi “Preparation”
     Ili ibada iweze kuwa na maana inahitaji maadalizi ya kutosha ni lazima viongozi wachukue hatua za kuiandaa ibada kulingana na vigezo hivyo hapo juu, kiongozi wa ibada na waabudu ni lazioma wajiandae wenyewe, baadhi ya maanadalizi ni ya kimwili si unajua si vema mtu kuhudhuria ibada akiwa amechoka mwili na akili au wanasinzia ibada nzima hii itawafanya kuwa nusunusu kwenye uwepo wa Mungu swala kama hilo ni chukizo la uharibifu kwa Mungu tunaye muheshimu sana
     Ingawaje maandalizi makuu ni maandalizi ya rohoni, kila mwabudu anapaswa kuziandaa akili zake na moyo wake kwa ajili ya ibada, Fanya tafakari, omba na jikabidhi kwa upya hapo mwabudu atakuwa amejikita katika katika mkondo wa upendo ambapo atapata uzoefu mpya wa nguvu za kiroho unafikiri nini kitatokea endapo itatokea katika ibada wahusika wakaomba kwamba Roho wa Mungu ashuke katika mkutano uliokuwa ukimsubiri akashuka kwa hakika ibada itakuwa yenye kuvutia sana.
2.       Hakikisha watu wanajihusisha “Participation”
    Jambo la muhimu sana katika ibada ni kuhusisha watu , kila mtu ni lazima ahusike katika kuabudu kama mtu atakuja katika ibada kama mtafiti tu  atakuwa amekoma kuabudu, bahati mbaya tuliyo nayo ni kuwa watu wengi huja ibadani kama watafiti au wachunguzi tu, mtu anafanya kazi ya kuangalia huyu kavaa nini , hapa wanaimbaje, kwaya ikoje , muhubiri kahubirije  matokeo yake hawaimbi, hawaombi, hawapokei ujumbe wa mahubiri, hawa ni wachunguzi tu wala sio waabudu, siku zote wito wa ibada ni kututaka tuhusike kikamilifu katika kuabudu kwenyewe ni lazima tukubali kushiriki ibada na kufikia hata uwezo wa kusema wimbo ni wimbo wangu nitauimba, maombi ni maombi yangu nitaomba ,sadaka yangu nitaitoa kwa Bwana, maneno ya Mungu ni maneno ya Mungu wangu kwangu ni ujumbe wangu aseme nami nitaupokea tu tabia kama hii na mtazamo kama huu unaifanya ibada iwe na maana
3.       Hakikisha ibada inaheshimika “Reverence”
     Heshima bado ni moja ya misingi muhimu ya ibada  Bwana Mungu wetu anaabudiwa , ni wakati wa utulivu wa kujali, kuhusika na kujitiisha, wako watu wana weza kuja ibadani na mambo ya mitaani wako ibadani lakini akili zao haziko pamoja na Mungu wanasahau kuwa wako nyumbani mwa Mungu, kuwa katika uwepo wa Mungu na kuwa nyumbani mwake hakuna tofauti kubwa  Mungu ni Mungu na hakuna Mungu mwingine aliye kama yeye  unawezaje kuwa mbele ya mfalme wa wafalme wa dunia nzima na mbingu na bahari kisha ukawa mapepe, kumuabudu Mungu katika kweli ni pamoja na akili zetu  na mawazo yetu na kumpa yeye Nafasi kwa kadiri iwezekanavyo hii inaleta maana pale unapo inama mbele zake kwa utulivu na unyenyekevu mkubwa jambo hili sisi wapentekoste hulipuuzia sana kama hakuna unyenyekevu na heshima na kumaanisha katika kuabudu basi hakuna ibada.
Jinsi ya kupanga ibada
    Jinsi tunavyopanga ibada inategemea na aina ya urithi wa mpango kamili wa ibada na mashauri kuhusu namna ya kushiriki ibada kama yalivyojadiliwa, Hali ya kupangilia ibada katika muonekano huu wa kawaida wa kuonekana kwa macho unapaswa kuchunguzwa uweje sasa hii ni kwa sababu mpaka mwaka wa 200 B.K yaani baada ya Kristo wakristo bado walikuwa hawajaanza kuabudu katika majengo kama tuliyo nayo leo wao walikutana pale gorofani, kwenye mapango na kwenye makaburi au sehemu zozote ambazo wangepata utulivu bila muingiliano wa mambo mengine , Nyumba za kuabudia wakristo zilipoanza kujengwa  zilikuwa rahisi na zenye kufanana na masinagogi ya kiyahudi baada ya hapo jengo lililofuata lilikuwa ni jengo la Roman basilica ambalo lilijengwa kama hall (Jengo hili liko katika makazi ya Pope huko Vatican) lakini kanisa lenyewe lilikuwa rahisi tu na hata ingawaje bado kuna majengo tofauti tofauti leo lakini mengi ni ya kawaida  wabaptisti kwa mfano hutenga madhabahu ya neno na meza ya kuwekea meza ya Bwana kwani wao huona kuwa kiini kikuu cha ibada ni Neno la Mungu vyovyote iwavyo muundo wa jengo na mitazamo ya waamini wa mahali hapo inaweza kuamua ni namna gani wajipange wakiabudu, hata hivyo ni muhimu kutotilia maanani maswala ya alama fulani fulani na pia kama watu wa mahali fulani wataamua kulifanya Jengo lao kuwa lenye thamani hawagombwi kufanya hivyo lakini wamishionari wa zamani walijenga vijengo kilingana na mahitaji ya mahali na kwa kusudi la kukusanyika na kukutana na waamini hivyo majengo mengi yalikuwa rahisi tu.
SURA YA SITA MUZIKI NA KUABUDU.
     Kusifu na kuabudu kwa njia ya muziki ni mapokeo tuliyoyapokea wakristo kwa wingi na utajiri wake kutoka katika dini ya wayahudi ambao wana utajiri wa ajabu kutoka katika maandiko na kusifu na kuomba na kuabudu tangu zamani, kwa karne nyingi wayahudi wamekuwa na ujuzi wa kutosha katika kumsifu Mungu aliye hai  hususani kwa kuimba,Uimbaji huo uliambatana na vyombo mbalimbali vya muziki na uliwashirikisha watu wote, Ukristo uliposhika kasi kusifu kwa njia hiyo kulikuwa ni sehemu ya ibada zao watu wote waliimba na zaburi zilikuwa ndio kama kitabu chao cha nyimbo ingawaje wakristo waliziimba zaburi katika maana nyingine mpya kwani Mungu waliyekuwa wakimsifu wakati huu alikuwa amekuja kuwaokoa kupitia Yesu Kristo
Kuabudu Kwa njia ya Muziki ni Urithi
     Wakristo walianza mara moja kutumia zaburi na hii ilikuwa ni kawaida ya maswala ya ibada za katika masinagogi ingawaje matumizi ya zaburi hizi zilikuwa na maana pana zaidi kutokana na wakristo kuamini katika ukombozi na umasihi wa Yesu. Kwa mfano Yesu Kristo mwenyewe katika karamu yake ya mwisho na wanafunzi wake aliimba Zaburi Marko 14;26, Tabia hii iliendelezwa na wakristo wa nyakati za kanisa la kwanza Baadhi ya wasomi huamini pia katika nyimbo zilizomo ndani ya agano jipya kama ule wa Zakaria, Mariam, na simeoni  na pia kuna salamu za neema ambazo zilitumika katika ibada, Aidha inasemekana Pia Paulo alinukuu baadhi ya nyimbo zilizokuwa zikiimbwa wakati huo mfano katika Waefeso 5;14 na ule wa 1Timotheo 3;16
kwa kuwa nuru ndiyo hufanya kila kitu kionekane. Hii ndiyo sababu imesemekana:
“Amka, wewe usinziaye,
ufufuke katika wafu,
Na Kristo atakuangazi.”
Bila shaka yo yote, siri ya utauwa ni kubwa:
Alidhihirishwa katika mwili wa kibinadamu,
alithibitishwa kuwa na haki katika Roho,
akaonekana na malaika,
akahubiriwa miongoni mwa mataifa,
akaaminiwa ulimwenguni,akachukuliwa juu katika utukufu.
     Hizo ni baadhi ya nyimbo ambazo zilikuwa zikiimbwa nyakati za kanisa la kwanza na inaonekana pia mitume walihimiza swala zima la uimbaji wa namna mbalimbali mfano ni katika Waefeso 5;19 na katika wakolosai 3;16 lakini baada ya kipindi fulani katika kanisa uimbaji wa jumla ulikoma  mpaka wakati wa mageuzi ya kiprotestant ndipo  uimbaji ulirejezwa kwa watu,  Moja ya nyota wa kimapinduzi wa uprotestant John Huss wa Bohemia  alianzisha uimbaji na kuchapisha kitabu cha uimbaji mwaka wa 1501, Martin Luther pia alisisitiza sana uimbaji wa jumla  na aliandika nyimbo zaidi ya 30 na hivyo mpaka mwaka 1552 waluther walikuwa ni waimbaji wakubwa sana na uimbaji tulionao leo ni matokeo ya uimbaji uliotokea wakati wa uamsho wa Isaac Watts na John na Charles Wesley uamsho wa wakati wao huko Uingereza na uamsho mkubwa wa huko Marekani  vyote vilichangia aina za uimbaji tulio nao leo.
     Katika Agano la kale na jipya Muziki ulikuwa ni sehemu muhimu sana ya kumuabudu Mungu, kwa mfano katika agano la kale wao walichagua waimbaji kwa uangalifu mkubwa sana ili kuongoza watu katika kufurahia kuabudu 1Nyakati 15;16-22 jamii ya waimbaji na watu wa muziki walichaguliwa kutoka miongoni mwa familia za kabila za kikuhani yaani walawi watu ambao walikuwa wamewekwa wakfu kwa ajili ya utumishi wa Mungu na waliofunzwa kwa ufanisi maswala ya muziki, Sasa tunaishi katika ulimwengu wa Muziki duniani kuna kila aina za uimbaji Ndege wanaimba na kuna sauti za kila aina za kufurahisha haishangazi endapo muziki huo utaimbwa kutoka katika hisia za ndani sana za pendo la Mungu jambo la kumsifu Mungu kwa njia inayoambatana na muziki linampendeza Mungu sana Zaburi 147; 1 inasema “Tazama jinsi ilivyo vyema kumwimbia Mungu wetu sifa,
jinsi inavyopendeza na kustahili kumsifu Yeye! ”
     Kusudi la msingi la Muziki ni kwa ajili ya kumuabudu Mungu na kumsifu yeye, Muziki umekuwa ni msaada wa karibu sana katika swala zima la kuabudu unasaidia sana watu kumuabudu Mungu, Biblia inatoa mifano mingi sana ya matumizi ya vifaa vya muziki na sauti stadi kwa msingi huo tunajifunza umuhimu wa kuabudu kupitia muziki, msisitizo mkubwa wa kuabudu kwa kutumia vyombo vya Muziki umetolewa katika agano la kale zaidi kuliko katika agano jipya Biblia inanukuu matumizi ya kwanza ya muziki kwa kuonyesha vyombo vya muziki Mwanzo 4;21 vyovyote Biblia inavyosisitiza swala zima la Muziki na vyombo vya muziki kusudi kuu ni kuabudu na kumsifu Bwana
 Je Muziki katika Ibada ni dhambi?
     Muziki ni wa muhimu kwa kila tamaduni kwani unawakilisha mawazo na hisia za watu sawa na tamaduni zao, kwa hivyo lazima muziki utunzwe katika tamaduni ya mahali hapo kwa gharama yoyote, tunapojifunza umuhimu wa muziki na nafasi ya muziki katika maisha ya watu tutaanza kupata picha kwa nini ni muhimu kutunzwa kwa gharama yoyote, Muziki ni moja ya alama za kawaida katika tamaduni zote kila aina ya kabila duniani wana aina zao za Muziki na katika tamaduni nyinginezo muziki huambatana na maswala ya kuabudu kadiri ulimwengu unavyokua kumekuweko na mwingiliano wa tamaduni za kimuziki na hivyo Muziki wa kanisa umetoka nje na kuathiri baadhi ya tamaduni na miziki ya baadhi ya tamaduni imeingia kanisani au kuchanganyika na  ya jamii nyingine kwa hivyo sasa Muziki hauna mwenyewe
     Mungu aliutumia Muziki kama njia ya kurithishana mafundisho toka kizazi hata kizazi hii iko wazi katika Kumbukumbu la torati 31 na 32 kabla kidogo ya kifo cha Musa Mungu alimwambia Musa sasa jiandikie wimbo huu na uwafundishe wana wa Israel wimbo huu utawashuhudia  kwa sababu hautasahaulika na vizazi vyao Kumbukumbu 31;19,21;32 44-47.
     Kwa msingi huo basi hatuwezi kuhukumu kuwa aina fulani ya muziki ni dhambi kwani muziki unatokana na tamaduni mbalimbali na historia na unatofautiana kulingana na maeneo mbalimbali na makusudi mbalimbali lakini linapokuja swala la kuabudu bila kujali ni aina gani ya muziki inapigwa mambo kadhaa ya msingi ni laziama yazingatiwe ili kuifanya ibada iwe ibada na iweze kuwa tofauti na makusudio mengine ya muziki mambo ya kuzingatia ni pamoja na ;-
·         Wimbo wa kusifu na kuabudu ni lazima umtukuze Mungu- Ibada ya kweli huleta furaha na Mungu anataka watu wawe na furaha hakuna ubaya kuwa na hisia nzuri ingawaje miziki mingi haijali kitu kuhusu Mungu wala haitupi hisia kuhusu Mungu kwa msingi huo hata kama muziki huo utakuwa mzuri na wenye hisia kali lakini kama hauusu Mungu katika kuabudu Muziki huo haumpi Mungu utukufu.
·         Wimbo wa kusifu na kuabudu lazima uwe unatoka moyoni kwa kumaanisha- kama kumsifu kwetu Mungu na kumuabudu hakutokani na ukweli kutoka moyoni Mungu hawezi kufurahia nyimbo zetu Nabii Amosi alikemea maswala ya unafiki wa wayahudi waliokuwa wamerudi nyuma na kumuacha Mungu lakini waliendelea kufanya ibada lakini hawakumaanisha kile walichokifanya bali walifikiri mambo mengine Mungu hapendezwi na ibada za namna hiyo Amosi 5;23
·         Wimbo wa kusifu na kuabudu lazima useme kile maandiko yanachokisema- ni muhimu kufahamu kuwa uimbaji ni muhimu pia ukaimbwa sawa na mafundisho sahii ya Biblia kwa mfano mtu anaweza kutunga Nyimbo inayosema kuwa wakristo tutawekwa huru mbali na majaribu ya kila aina lakini maandiko yana sema tutajaribiwa 1Petro 1;6-7 wimbo wa aina hiyo utakuwa haukuzingatia uwiano wa maandiko haufai, Muimbaji anaweza kuwa mwema na mwaminifu lakini wimbo hauko sawa na mafundisho ya Biblia  kwa msingi huo ni lazima wimbo uzingatie kuwa baraka na sio kuwapotosha watu kutoka katika neno la Mungu ushauri wa bure kwa waimbaji wa nyimbo za injili kwenda kusoma katika vyuo vya biblia kwao ni muhimu sana ili waimbe sawa na tafasiri halali za maandiko.
·         Wimbo wa kusifu na kuabudu lazima uguse mahitaji mbalimbali ya watu – Ni muhimu pia nyimbo zikagusa mahitaji ya watu pamoja na shuhuda zao wimbo unaoongoza watu kuabudu siku zote uendane na makusudi ya kuabudu kwenyewe kwa msingi huo tunapoimba na kusifu yale ambayo bwana ametufanyia ni sehemu ya shukurani kwetu, na uchaguzi wa nyimbo unapofanyika lazima uzingatie lile kusudio la wimbo na mahitaji ya watu na wakati
·         Wimbo wa kusifu na kuabudu haupaswi kuwatoa watu katika kusudi la kuabudu- watu huabudu vema sana na wimbo wanaoufahamu kuliko wimbo mpya ingawaje ni vema kujifunza wimbo mpya ili kwamba ibada isiwe yenye mazoea lakini jambo la msingi ni kuwa lisiwachukue watu nje ya kusudi la kuabudu Mungu na utukufu wake ni lazima vipewe kipaumbele kama kiini cha ibada
Aina mbalimbali za kusifu.
     Kutokana na vyanzo mbalimbali vya urithi wa Muziki kumekuweko na aina mbalimbali za kusifu ujuzi kuhusu aina mbalimbali za kusifu utamsaidia kila kiongozi wa ibada kutumia sauti na vyombo kusaidida katika kumuabudu Mungu kwa namna mbalimbali tulizo nazo
Kianzilishi
     Ni aina ya muziki wa mwanzoni ambao unaweza kupigwa au aina ya sifa ya mwanzo ambayo inaweza kutolewa kama kiashiria cha kuwa ibada inaanza nyimbo hizo za uanzilishi zinapaswa kuwa zenye kutengeneza mazingira ya kumuandaa muabudu kujua kuwa ibada sasa inakaribia kuanza au inaanza
Wito wa kuabudu
     Huu ni wimbo wa kuabudu au sifa amabao unamkubusha mwabudu kuwa amweke Mungu kati sasa kama kiini cha kuabudu, wimbo wa aina hiyo utawajulisha watu kuwa Bwana yu hekaluni mwake au utaita watu kuabudu na kujihusisha katika kuabudu
Mwitikio
     Hii ni aina ya sifa inayoonyesha mwitikio inawezekana yakawa ni maombi na watu wakaitikia amen hili ni itikio la kuonyesha kuwa Mungu ameitikia maombi yao
Vyombo vya Muziki
Zinaweza kupigwa ala fulani za vyombo vya muziki au muziki maalumu unaoashiria kuinua mkutano katika kumsifu na kumuabudu Mungu Muziki wa aina hiyo uwe unampa Mungu utukufu ama munaweza kuimba wimbo
Kuabudu sio tu kuko kwa namna nyingi lakini pia ni lazima kuweko na viini vya kuabudu wakati wa kutumia Muziki viiini hivyo ni pamoja na
Ø  Swala zima la kuabudu
Ø  Kumuabudu Mungu baba
Ø  Kumuabudu Bwana Yesu
Ø  Kumuabudu Roho matakatifu
Ø  Kufundisha neno la Mungu
Ø  Kuzungumzia wokovu
Ø  Kukumbusha maisha ya kikristo
Ø  Kukumbusha wajibu wa kanisa
Ø  Kuhusu ufalme wa Mungu
Ø  Kuhusu umishenari
Ø  Kuhusu jamii bora
Ø  Kuhusu maisha ya milele
     Lakini ni muhimu pia unapoimba kuhusu wokovu  kukumbushia swala la wokovu kwa neema, toba na maungamo ya kweli na wito wa kukubali na unapozungumzia maisha ya ukristo  unaweza kukazia imani, uhakika, tumaini, upendo, amani na faraja, furaha, maombi, kujiwejka wakfu, ushirika  na maisha bora ya wakristo majumbani mwao
Sifa za Muziki unaofaa katika kumsifu Mungu
*      Unaokubalika kitheolojia
*      Rahisi na wenye lugha ya kueleweka
*      Unaoimbika
*      Unaoeleweka
SURA YA SABA BIBLIA NA KUABUDU
    Maandiko yamekuwa siku zote ni ya lazima ya muhimu katika swala zima la kuabudu Kikristo, Nyakati za kanisa la kwanza wakristo walipokuwa wanakutana walichagua maandiko ya kusoma kutoka agano la kale na baadaye injili zilipoandikwa na nyaraka nazo zilianza kusomwa, Na kwakuwa tangu awali kuabudu kwa kikristo kulikuwa ni pamoja na kusikia Neno la Mungu linasema nini Maandiko yamekuwa ni sehemu muhimu ya kila ibada ya kiagano jipya,Unapoipitia Biblia utaweza kuiona inapotumika kwa ibada na itakupa mwanga wa aina mbalimbali
1.       Inatoa mwito wa kuabudu
2.       Inatupa mafundisho
3.       Inaweza kutumika katika kutoa baraka na kutoa neema mwishoni mwa ibada Hesabu 6;22-27,2Koritho 13;14,Warumi 16;24,Wagalatia 6;18,Efeso 6;23,1Tomotheo 6;20-21 ni maandiko yanayotumika sana kwa salamu za neema au baraka baada ya ibada
4.       Inatumika kwa ajili ya Mahubiri na usomaji wa maandiko.
Namna ya kuisoma Biblia katika kuabudu
1.       Pangilia namna ya kuisoma Biblia kwakuwa Biblia hutumiwa na watu wengi katika maswala ya kuabudu ni muhimu basi kwa kiongozi wa Ibada kujiandaa au kuandaa sehemu za maandiko ya kuyasoma ,si jambo la kushangaza kuwa kuna watu wanaweza kuisoma Biblia na kuipenda inaposomwa lakini kuna uwezekano wasiweze kujua sura aya na hata kitabu  kwa msingi huo maandalizi ni lazima yafanyike kuandaa wapi pa kusoma au vifungu vya kusoma ili kwamba kama watu wamekuja na Biblia zao waweze kufuatilia  kwani wasipojua ni kitabu gani kinasomwa na ili waweze kufuatilia aidha ni muhimu pia kuelezea kuwa ni toleo gani linatumika ili wafuatiliaji waweze kujua ni Biblia toleo gani inatumika
2.       Biblia isomwe kwa sauti biblia ni muhimu ikisomwa kwa sauti ya kueleweka kwa uwazi na maana yake ni lazima ieleweke, yaani maana ya kifungu kinachosomwa  kwa msingi huo kifungu cha maandiko kinachosomwa wakati wa kuabudu ni lazima kieleweke na kusomwa kwa sauti safi na na inapowezekana anaweza kurudia mara mbili, wakati Ezra na waandishi walipokuwa wakisoma sheria pia ilikuwa ikirekodiwa pia na kufafanuliwa  ili kwamba watu waweze kuelewa kile kilichokuwa kinasomwa Nehemia 8;8 aina hii ya usomaji wa maandiko ni muhimu ikifuatwa.
3.       Usiisome Biblia kupita kawaida Do not overread ni muhimu kufahamu kuwa si vema sana kuisoma Biblia kwa mtindo wa kuiigiza au kuisoma kwa namna ambayo itawatowa watu katika usikivu wa kwamba wanasoma Biblia  lakini isomwe katika namna ambayo watu watajua kuwa inayosomwa ni Biblia iadha msomaji anapiosoma asababishe watu waone jinsi Biblia ilivyo ya ajabu na nzuri na sio waseme jamaa anasoma vizuri sana, Biblia isomwe katika misisitizo yenye kufundisha maana  au kukazia maana  ili kuipa nafasi ionyeshe kile inayosema , Biblia inaweza kuwa sauti ya Mungu kwa watu wake  na hivyo isomwe katika namna ambayo watu wataona kuwa Mungu anasema na watu wake
4.       Biblia ndio kiini kikuu cha ibada kwa msingi huo sio tu Mungu huzungumza kwa usomaji wa maandiko lakini pia kupitia mahubiri hapo huzungumza na watu aliowaita  hivyo Mungu pia huzungumza na watu wake kupitia neno lake linapohubiriwa na wahubiri
a.       Kiini cha mahubiri- Mahubiri ya Kikristo ni tofauti na mahubiri ya desturi nyingine kwa ufupi mahubiri ya Kikristo mwanzoni hayakuwa yenye kufurahisha sana kwani wanafalsafa walikuwa na wasemaji wao waliokuwa wasemaji hodari aidha wayahudi pia walikuwa na wahubiri wao maalumu  lakini katika ukristo kiini kilikuwa si wasemaji hodari bali ujumbe na mwanzoni injili ilikuwa ni tangazo kuwa Mungu yu awakomboa watu wake na mahubiri yalitokana na nguvu za Roho Mtakatifu na ujumbe aliowapa katika mioyo yao, Yesu alikuwa muhubiri wa kawaida aliyekuwa akitembea huko na huko akihubiri habari njema kwa watu wa kawaida  na kila mtu alimwelewa aidha aliwatuma wanafunzi wake kuhubiri na mwisho aliacha agizo kwa watu wote kuhubiri, kuhubiri ilikuwa ni kiini cha ujumbe wa Mungu kuwafikia watu na mwito wa watu kufikiwa na injili ili wakombolewe Warumi 10;14 kwa msingi huo kiini kikuu cha mahubiri ni kufikisha habari za ukombozi kwa watu wa Mungu kwa njia ya upumbavu yaani iliyodharaulika kanisa la kwanza watu walikuwa na utiliaji maanani mahubiri ya aina hiyo kwani kukosekana kwa hilo kunaweza kuyafanya mahubiri yasiwe na maana jambo ambalo linaikumba jamii yetu leo katika mahubiri sio sehemu ya kuonyesha uwezo wetu wa kujieleza au kunena bali kumtangaza Mungu ili kwamba tabia na mwenendo wa watu uweze kuguswa na kubadilika kumuelekea Mungu Mtu mwenye ujumbe wa Mungu huwa na mvuto wa tofauti na kuwafanya watu wavutike kutaka kusikia Mungu anazungumza nini nao sio namna unavyovaa au muonekano Luka 7;24-29 ujumbe wa Yohana uliweza kubadilisha maisha ya watu wengi waliohesabika kama wenye dhambi na kuwaacha wale tu wenye kiburi na kujihesabia haki yaani mafarisayo
b.      Asili ya mahubiri- Kama kuhubiri ni muhimu sana basi lazima asili ya kuhubiri ieleweke vema mahubiri asili yake lazima itoke katika mawazo ya Mungu, mahubiri hayapaswi kuwa asili ya muhubiri, maoni au mtazamo wake bali ujumbe wa Mungu kwa msingi huo muhubiri lazima awe na uwezo wa kupokea mawazo ya juu sana ambayo ni mawazo ya Mungu Isaya 55;9, “Mawazo yenu si mawazo yangu ….” Kwa msingi huo uhusiano wa  maandiko na ujumbe utaonekana  ukijengwa katika maandiko hii ikiwa ni pamoja na utoaji wa mifano itakayoendana sawa na kiini cha ujumbe uliokusudiwa  kwa maana nyingine mahubiri ni sauti ya Mungu na ili mtu ahubiri sauti ya Mungu Mwanatheolojia Donald Miller alisisitiza hivi “Mahubiri ya kweli lazima yawe yanafunua biblia (Expository Preaching) na mahubiri yasiyiofunua biblia(Expository Preaching)  hayo siyo mahubiri”ingawaje kauli hii inaweza kuwa imevuka mipaka kwani kunaweza kuweko mahubiri ya kibiblia yasiyo funua Expository lakini mkazo ukawa ni kweli ya kibiblia  jambo la msingi ni muhubiri kuisoma Biblia kutambua kiini  na kuhubiri kwa makutano
c.       Mahubiri Kama sehemu ya ibada- kuna uhusiano kati ya mahubiri na ibada na mahubiri ni ibada au sehemu ya ibada kuna maoni mbalimbali yanayotolewa kuhusu uhusiano wa mahubiri na ibada
*      Kuna wanaofikiri kuwa mahubiri sio ibada  hili ni kundi la wakristo wanaoona kuwa mahubiri sio ibada  na huyavumulia tu kwa mazoea  na ziko sehemu nyingine ambazo mahubiri yamekuwa yakikimbiwa au kuachwa na watu yanapoanza tu watu huondoka zao wakifikiri kuwa sio sehemu ya ibada baadhi ya madhehebu kama Anglican na Roman catholic waliamua kuyaondoa au kuyaweka kwa kiasi sana au kuyaondoa kabisaa katika taratibu zao za ibada ikifikiriwa kuwa sio sehemu muhimu ya ibada ingawaje makanisa mengi ya kiinjili huona mahubiri kuwa sehemu muhimu ya ibada.
*      Kuna wanaoona kuwa mahubiri ni sehemu ya ibada iliyo ya muhimu sana  hawa ni baadhi ya wakristo au madhehebu ambayo huona kuwa mahubiri ndio sehemu muhimu sana kuliko zote katika ibada imefikia hatua ambayo wengine hawahudhurii ibada isiyo na mahubiri au wengine hufikia hatua pale wanapokuwa wamechelewa mambo mengine kama sifa n.k. lakini mahubiri akayawahi huona kuwa hajachelewa kitu kwani amewahi mahubiri hili ni kosa kwani ibada ni kiini kikuu cha kuabudu na hivyo kila sehemu ya ibada ni sehemu ya kuabudu pia hivyo hakuna sehemu iliyo muhimu kuliko nyingine zote ni sehemu za ibada na matendo yote kwa ujumla ndio hufanya jumla ya kuabudu.
*      Mahubiri ni sehemu ya ibada tunaweza kujiuliza swali na kujijibu kuwa ni nini umuhimu wa mahubiri? Mahubiri ni sehemu ya ibada  ni tendo la kuabudu hata ingawaje ni sehemu muhimu ya ibada lakini sio sehemu ya pekee ya ibada kwani maombi, nyimbo, u somaji wa maandiko na utoaji wa sadadka ni sehemu za muhimu za ibada, mahubiri ni ya kwanza miongoni mwa hayo na hivyo ni lazima yawe msingi na kilele cha ibada  lakini kamwe hayawezi kusimama peke yake tu  ni moja ya matendo ya kuabudu miongoni mwa mengi yaliyo sawa na kwakuwa  kuhubiri ni kutangaza ujumbe wa Mungu basi jaribio lolote lile la kupunguza au kutenganisha matukio mengine na mahubiri ni upotevu wa misingi ya ibada  kwani katika kuabudu Mungu husema na wanadamu husikia  na muhubiri anapohubiri Mungu huzungumza na hiyo ndiyo ibada ya kweli
*      Mahubiri na meza ya bwana
Baadhi ya wanatheolojia hawakubaliani na wazo la kuwa mahubiri ni kiini kikuu cha ibada na badala yake wao huona kuwa kiini kikuu cha ibada ni Meza ya bwana au Ekaristi kabla ya kukubali au kukataa wazo lao agizo kuu kuhusu kuhubiri injili liliambatana na neno fanyeni hivi kwa ukumbusho wangu, Ni muhimu kufahamu kuwa meza ya bwana ni miongoni mwa tangazo la kifo cha Bwana Yesu sio tu ni miongoni mwa tangazo lakini haionekani kuwa ndio ya msingi wa utangazaji injili katika agano jipya.Swala la meza ya bwana ni tukio la kikuhani zaidi katika historia za kibiblia Yesu alifanya kazi kubwa ya kinabii na kichungaji zaidi kuliko ya kikuhani kwa hiyo ni muhimu kufahamu kuwa Mungu kupitia mwana wake Yesu Kristi ndio njia kuu ya kupata neema  na sio meza ya Bwana  kama mtu atakazia kuwa meza ya bwana ni sehemu ya neema na ya muhimu kuliko Kristo mwenyewe itakuwa ni imani nyingine potofu au injili nyingine kwa hiyo ulingano ulio sahii kati ya mahubiri na meza ya Bwana ni muhimu ukawekwa sawa mapema kila moja lina sehemu katika ibada unaweza kutoa umuhimu kwa meza ya bwana bila kuacha meza ya bwana kuchukua nafasi ya mahubiri jambo la muhimu kufahamu ni kuwa meza ya bwana ni moja ya njia ya kuhubiri au kutangaza kazi ya ukombozi iliyofanywa na Mungu
d.      Wajibu wa waamini  kama sehemu ya mahubiri
Waamini wana wajibika kuhusika kutimiza sehemu yao kama sehemu ya mahubiri hayo wajibu huu ni zaidi ya kuonyesha mwitikio wa ujumbe wakati wa mahubiri, wajibu mmoja wa waamini ni kwanza kukumkubali muhubiri na kumuona kuwa ni mmoja wa watu waliopakwa mafuta na Mungu waliseme neno lake au kuleta ujumbe kwao na ujumbe wake ni muhimu ukipokelewa kama ujumbe wa Mungu jambo kama hili likijengeka litawawezesha waamini kukaa kwa usikivu na utii , 1Wathesalonike 2;13 “Kwa sababuhiyo sisi nasi twamshukuru Mungu bila kukoma kwa kuwa mlipopata lile neno la ujumbe la Mungu mlilolisilkia kwetu mlilipokea si kama neno la wanadamu, bali kama neno la Mungu ;na ndivyo lilivyo kwelikweli litendalo kazi ndani yenu ninyi mnao amini”  kwa msingi huo pia ni wajibu wa waamini kuombea muhubiri kila wakati siku zote ili kwamba waseme ujumbe utokao kwa Mungu na kuwa hakuna mwenye haki ya kumkosoa muhubiri kama hukuhusika katika kumuombea 2Thesalonike 3;1 “Hatimaye ndugu tuombeeni…”lazima tusikilize neno katika hali ya kuomba  na mwisho tuitikie mwito wa mahubiri kwa hiyo basi Biblia ni moja ya sehemu muhimu ya ibada.
SURA YA NANE MAOMBI NA KUABUDU
     Maombi ni moja ya sehemu ya Muhimu sana ya kuabudu  Mtu fulani husema kuwa ndio roho ya kuabudu  kunauwezekano ikawa hivyo  lakini maombi ni moja ya sehemu ya ibada  yanamtambua Mungu kwa sababu yanaelekezwa kwake  yanasaidia kutuunganisha na Mungu kwani moja ya sababu ya kuishi kwetu ni ili tuunganishwe na Mungu  na nisehemu pia ya kumshukuru sana Mungu mara nyingi maombi pia yametumika kama sehemu ya siri ya uhusiano na Mungu  kwa msingi huo basi dakika anagalu kumi au kumi na tano hivi ya siku za jumapili ibadani ni muhimu zikitolewa kwaajili ya maombi tutayazungumzia maombi ya Binafsi kwa wakati wake lakini hebu tuzungumzie maombi ya pamoja
Asili ya maombi ya Pamoja.
     Asili ya maombi ya pamoja kwa ujumla haieleweki lakini maombi ya pamoja ni ya muhimu kuliko maombi ya binafsi katika maombi ya binafsi mkristo anakuwa hana mipaka anazungumza na Mungu kwa kadiri awezavyo kwa kufuata hali yoyote aitakayo lakini katika maombi ya pamoja kiongozi hufanya zaidi ya maombi ya mtu mmoja mmoja muombaji Binafsi anaweza kuombea yoyote ayatakayo lakini katika maombi ya pamoja hitaji fulani  moja huafanyika kwa ajili ya kuwakilisha watu wote waliopo au kanisa katika maombi ya Pamoja kiongozi hutaja hitaji kisha watu wote huombea pamoja na wakati mwingine kiongozi huomba kwa niaba ya watu wote
Aina mbalimbali za maombi.
Kumtukuza Mungu adoration
     Maombi ni njia mojawapo ya kumuabudu Mungu lakini kumtukuza Mungu ni moja ya njia muhimu sana za kumuabudu hii ni hali ya kumtukuza Mungu na kulisifu jina lake aina hii ya maombi ni ya lazima kwa sababu huwekwa mbele zaidi kuliko aina nyingine za maombi kwa kawaida maombi ya kumtukuza Mungu huwa ndo ya kwanza kumbuka msingi was ala ya Bwana unasema Baba yetu uliye mbinguni jina lako litukuzwe
Shukurani thanksgiving
     Maombi yanakwenda kilaini ikiwa baada ya kumtukuza Mungu unaunganisha na kushukuru kwani kumtukuza mungu huambatana na kumuinua na kukumbuka wema wake na upendo wake na fadhili zake ni kana kwamba mwabaudu anatambua kuwa bila Mungu hawezi kufanya jambo lolote anakumbuka zawadi nyingi au fadhili nyingi za Bwana, ikiwa pamoja na wokovu kupitia Yesu Kristo na neema yake ya ajabu kwetu ndipo sa tunajihisi kushukuru na kwa mambo mengine mengi swana
Toba au maungamo Comfession
     Aina hii ya maombi ni maombi ya toba au maungamo au kujitakasa Mungu wetu ni mtakatifu na kuwepo katika uwepo wake pasipo utakatifu ni kujiweka katika uhusiano mwema na yeye, Toba inasaidia kuleta mapatano na Mungu mara nyingi msamaha huu tunaouomba sio lazima iwe kwa ajili yetu tu bali na kwa ajili ya wengine kumbuka msingi katika sala ya bwana “Utusamehe makosa yetu…” ina weza kuwa toba ya dhambi Fulani maalumu katika kanisa kwa ujumla au kujiweka sawa kwa ajili ya kumkaribisha Mungu.
Dua Petition
     Dua ni sehemu ya maombi kuomba dua ni kumshirikisha Mungu mahitaji yetu aina hii ya maombi inaweza kusisitizwa katika msingi was ala ya Bwana tunaona maneno “utupe leo riziki yetu…” Mathayo 6; 11-13 na 7;7-8
Maombezi Intercession
      Maombezi yanafanana sana na Dua lakini maombezi ni kuomba kwa niaba ya aina hii ya maombi pia ni ya muhimu kutiwa moyo ni kuacha mahitaji yetu binafsi na kuinua mahitaji ya wengine kwa mujibu wa Yakobo maombi ya mwenye haki yafaa sana akiomba kwa bidii
Kujitoa Dedication
     Haya ni maombi ya kujitoa upya kwa Mungu kila wakati maranyingi aina hii ya maombi hutolewa mwishoni mwa kumalizia ibada.
Aina za maombi katika ibada
1.       Maombi ya ufunguzi
Kwa kawaida ni maombi yanayoombwa mwanzoni kwa ajili ya ufunguzi wa ibada lengo la maombi hayo ni kuziita Baraka za Mungu kumiminika katika ibada hayapaswi kuwa maombi yanayogusa kila sehemu ya ibada yanatakiwa kuwa ya kifupi na yenye viini viwili yaani kuabudu na dua ya kumuhitaji Mungu yanatakiwa yamtukuze Mungu na kuhiytaji Baraka zake kwaajili ya ibada
2.       Maombi ya kichungaji.
Maombi ya msingi sana mi maombi ya ibadani haya huitwa maombi ya kichungaji kwa sababu hutolewa na mchungaji ni maombi kwa ajili ya kondoo ni marefu kisi kuliko maombi mengine lengo lake kuu ni kushukuru, kuomba toba kwa ajili ya watu wote, dua na maombezi kwa ajili ya shida za watu wengi wa wachungaji huyafanya maombi ya jinsi hii mwishoni mwa ibada
3.       Maombi kwa ajili ya sadaka.
Hii ni aina ya maombi inayotolewa katika uhusiano na sadaka inweza kuwa kabla watu hawajatoa au baada ya watu kutoa maombi haya hulenga kubariki zawadi za watu walizozileta kwa Mungu
4.       Maombi baada ya mahubiri.
Ni aina ya maombi yatolewayo baada ya mahubiri watumishi wengi wa Mungu huombea watu baada ya mahubiri maombezi haya hulenga kjuombea watu toba, au magonjwa au kuhitimisha ibada au mahubiri na kujikabidhi tena kwa Mungu
5.       Maombi ya neema.
Ni maombi yatolewayo mwishoni kabisa mwa ibada kwa ajili ya kuwabariki watu ingawaje yanapaswa kuwa mafupi sana “Neema ya Bwana wetu Yesu Kristo na upendo wa Mungu Baba mwenyezi na ushirika wa Roho Mtakatifu ukae nanyi nyote amen”
NAMNA YA KUOMBA
Sio tu kwamba kuna aina tofauti za maombi lakini pia kuna aina tofauti za uombaji
1.       Maombi huria aina hii ya maombi katika ibada ni maombi ambayo kiongozi wa ibada anaacha kila mmoja ajiombee kwa namna iwayo yote atakayo au maarufu kama Roho atakavyokuongoza  haya ni maombi yanayotoka katika moyo wa muombaji na huomba kwa kadiri ya muda uliotolewa  aidha kunaweza kuweko na uingiliaji kati wa kiongozi wa ibada kuelekeza nini cha kuombea kama toba ,kujitakasa na shukurani kisha kila mmoja kujiombea kama atakavyo, aina hizi za maombi ndio maombi yaliyoombwa sana nyakati za kanisa la kwanza , inatumika na itaendelea kutumika  tatizo kubwa la maombi ya aina hii ni uwezekano wa kukosa utaratibu lakini ni maombi mazuri na yenye nguvu za Roho na uponyaji
2.       Maombi ya mpangilio ya jumla hii ni aina ya maombi ambayo huandaliwa kiongozi aweza kupangilia nini kiwemo katika maombi na namna gani atatumia aina za maombi katika ibada  anaweza kuandaa aina za maombi na kuyachanganua  wanaweza kuytaandika ubaoni au kuyasoma kwa waombaji ingawaje maombi haya ya mpangilio yaweza kuwa na tatizo la utumiaji wa akili zaidi lakini huingia akilini na kuonyesha umaana kwa wamini
3.       Maombi yaliyoandikwa hii ni aina ya maombi ambayo imeandikwa katika vitabu mfano ni sala ya Bwana ni miongoni mwa mifano ya maombi hayo
4.       Litania hii ni njia ya maombi ya dua inayotolewa  na kiongozi huku waamini wakiitikia  aina hii ya maombi ni kama maombi ya mapatano ambapo kiongozi husoma baadhi ya vifungu vya dua na kasha waamini huitikia inaweza kuwekwa katika mtindo wa kuimba hivi mfano wa maombi hayo ni kama litania iliyotungwa na Mwanatheolojia  T.B. McDormand ambayo alituna mfano wa litania kama ifuatavyo

Kiongozi;- Mungu mwema mpaji wa kila kilicho chema  na kila kilicho kamili ambaye kwa ukarimu wako  ulionyesha upendo wako kwa mwanadamu kwa kumuumba kwa njia ya ajabu na kumuokoa kwa mwana wako Yesu kristo bwana wetu ee bwana usikie kuomba kwetu
Waamini;- Pokea shukurani zetu ee Bwana kilio chetu kikufikie
Kiongozi;-Kwa hakika umeamuru majira na nyakati duniani umetupa chakula mali na watoto ee bwana usikie kuomba kwetu
Waamini;- Pokea shukurani zetu ee Bwana kilio chetu kikufikie
Kiongozi;- upendo wako kwa wenye dhambi, wadahaifu na  kujali kwako wanadamu  na kwa neema na rehema zako kupitia mwokozi wetu kwa imani tunakuwa washindi zaidi ya kushinda  dhambi na mauti ee bwana usikie kuomba kwetu
Waamini;- Pokea shukurani zetu ee Bwana kilo chetu kikufikie
Mwishoni kwa pamoja waamini wote humshukuru Mungu.
5.       Maombi ya kukemea ni aina nyingine ya maombi ambayo pia kiongozi wa maombi huingilia kati kutoa maelekezo ya nini cha kuombea  anweza kusema hebu na tuombe kwa ajili ya wagonjwa na kisha kila baada ya maombi watu wanaamuriwa kukemea  kwa nguvu utendaji wa ibilisi wakitumia mamlaka waliyopewa  na kuangusha ngome na kuyteka nyara kila fikra ipate kumtii Kristo ni maombi yenye nguvu na uweza na kila muamini hufurahia Baraka za kiroho anapoomba aina hii ya maombi
6.       Maombi ya kimyakimya hii ni aina ya maombi ambapo kiongozi wa ibada ataruhusu mkutano kuomba kimyakimya  ingawaje aina hii ya maombi inahitaji inahitaji kutoa muda wa kutosha  kwa msingi hiuo maombi hayako katika mfumo wa aina moja ya maombi kuna hazina kubwa sana ya aina za maombikwa msingi huo inashauriwa kutumia aina mbalimbali za maombi na sio aina moja tu ya maombi ikakazaniwa
Mambo ya kuzingatia ni kuwa
-          Kiongozi wa maombi anaweza kuwa mchungaji au mtu yeyote mwenye ukomavu wa kiroho kama mashemasi au wazee wa kanisa wanaweza kuongoza maombi
-          Maombi yatolewe katika namna ambayo ni rahisi kwa waamini kukumbuka
-          Sauti katika maombi iwe yenye kusikika
-          Maombi lazima ikumbukwe kuwa yanaelekezwa kwa Mungu na sio kuzungumza kitu kuhusu Mungu kwani kuna wakati wa kuhubiri na wakati wa kuomba   
SURA YA TISA MAHALI PA KUABUDU.
     Nyakati za Agano la kale kazi ya kuabudu ilifanyika katika hema ya kukutania, mahali hapa uwepo wa Mungu ulipafunika na ile hema ikajawa na utukufu wa Mungu Kutoka 40; 34-35, Baadaye Mfalme Suleimani alijenga Heakalu la kwanza kabisa la kuabudia katika agano la kale na alipolikamilisha alipaita mahali akaapo Mungu 1Wafalme 8;10-12 Kisha akaomba dua hii
      “Lakini je Mungu atakaa duniani? Mbingu nahata mbingu za Mbingu haziwezi kumtosheleza jinsi gani hekalu nililojenga lilivyo dogo kwake Lakini sasa ee Bwana uisikie dua ya mtumwa wako niombayo Kwa rehema zako ee Bwana Mungu usikie kilio cha mtumishi wako na maombi ya mtumishi wako ninayoyaomba hivi leo, Macho yako yafumbuke kulielekea hakalu hili usiku na mchana, mahali hapa ulipopatakja ukasema, ukasema hapa ndipo litakapokuwako jina langu ili uyasikie maombi ya mtumwa wako aombapo akikabili mahali hapa, uisikie dua ya mtumwa wako nay a watu wako Israel watakapoomba wakikabili mahali hapa naam sikia huko mbinguni nawe usikiapo samehe….” 1Falme 8;22-53. Nyakati za agano la kale Mungu alichagua mahali ili apaweke jina lake hapo na mahali hapo watu wangeelekea kuabudu mahali hapo palikuwa ni lazima kwa ajili ya ibada mwanzoni Mungu aliagiza kuhusu Ujenzi wa hema ya kukutania kama mahali pekee pa kuabudia lakini baadaye Suleimani alijenga Hekalu na baada ya uhamisho wa babeli kulikuja maswala ya masinagogi ambayo kwa asili ndiyo yaliyotuletea makanisa pamoja na kuwa misnbgi wa ibada ni rohoni lakini kwa namna moja ama nyingine inatupasa kukusanyika kama ilivyokuwa nyakati za kanisa la kwanza Matendo 2;46, aidha Kristo mwenyewe ingawa alikuwa Mungu na alikuwa wa Kiroho kuliko mtu awaye yote hakuacha kamwe kuelekea katika nyumba za ibada Luka 2;49 aidha mitume na watakatifu waliotutangulia waliheshimu ibada za pamoja na saa maalumu zilizowekwa kwa ajili ya kuabudu Luka 2;36-37,24;53.Matendo 3;1,pia walifurahi kuweko nyumbani mwa Bwana zaburi 84;1-2,10 na 122;1 kwa nini Biblia inasisitiza kuelekea nyumbani kwa Bwana? Kumbukumbu la Torati 12; 25 “Lakini mahali atakapopachagua Bwana Mungu wenu….apaweke jina lake maana ni makao yake mahali hapo ni lazima uende” aidha inasisitizwa kuwa yusiache kukusanyika Waebrania 10;25 hivyo basi mahali pa kuabudu ni lazima kwenda.
Leo hii waamini wanaabudu katika nnjia iliyo bora zaidi kuliko zile za agano la kale lakini wapi ni mahali sahii pa luabudia leo? Leo hii ni muhimu kufahamu kuwa mahali pa kuabudia sio swala swala ni mkao wa mtu anayeabudu moyo wake ukoje? Hapa simaanishi kuwa yale majengo yetu tunayokutania kuabudiu yawe mabaya au yasiheshimike hapana Mungu ameweka jina lake hapo na ni lazima uende huko kuabudu lakini Muhimu ni mkao wa moyo wa muabudu na uhusiano wake na Mungu ulivyo mahali pa kuabudu pako na Yesu mbinguni soma Waebrania 3;6, na makao ya mungu leo ni watu wake Mungu sasa anafanya makazi katika mioyo ya wanadamu na ndio maana nakazia tena kuwa swala la ibada ni mkao wa moyo wa muhusika, Yesu alisema walipo wawili watatu wamekusanyika kwa jina langu name niko katikati yao unaona Mungu anaweza kuwako kokote pale ambapo watu wamekusanyika kwa ajili yake kwa faida yake kwa moyo unaoelekea kwake, kwa hivyo hata mtu binafis akitaka kuabudu anaweza kuabudu pake yake , lakini bado anapaswa kuyatiii maandiko kwani yanakazia kutokuacha kukusanyika.


Mahali pa kuabudu nyakati za agano la kale palikuwa ni mahali pa kuheshimika sana Kristo pia alikemea wale waliokuwa wakiidharau nyumba ya Mungu na kulifanya kuwa pango la wanyang’anyi hata leo tunapaswa kuendelea kuheshimu mahali panapofanyikia ibada bila kusahau mioyo yetu kuandaliwa kama sehemu muhimu ya ibada unaloliona ni mfano wa hekalu lililojengwa na Herode mkuu na kutumiwa wakati wa Yesu hii ni ramani yake huko Israel ikiwa imejengwa kwa mfano Picha na maelezo kwa hisani ya maktaba ya Mchungaji Innocent Kamote
SURA YA KUMI KUABUDU BINAFSI NA KUABUDU KIFAMILIA
     Ni muhimu sana pia kufikiri kuhusu kuabudu binafsi pamoja na kuabudu kifamilia  kwani vyote kwa pamoja vinakamilisha uabudu wa pamoja na ibada hizo zote ni muhimu kwa ajili ya kufikia kwenye cheo cha kimo cha utimilifu wa Kristo yaani ukuaji au ukomaaji wa Kiroho

Kuabudu Binafsi
     Kuabudu Binafsi ni kwa muhimu sana kwa ajili ya ukomaaji wa kiroho na kukua kiroho katika maisha, wakristo pia wanapaswa kutiwa moyo katika swala zima la kujihusisha na kuabudu binafsi  na kujitoa ingawaje hakuna mpangilio maalumu wa namna ya kuabudu kwa msingi huo namna ya kuabudu Binafsi inaachwa kwenye uwezo wa muhusika Binafsi kwani ibada binafsi ni maswala ya mtu binafsi na Mungu wake  na unapotoa Muongozo itakua ni swala la kukazia kulikopita mipaka  na itakuwa ni mapngilio wa swala la kidini zaidi kuliko uhusiano binafsi wa Mtu na Mungu wake ingawaje wale wenye tabia ya ibada binafsi na kujitoa wanaweza kuwa na vidokezo muhimu vinavyoweza kuwasaidia wengine katika tabia ya ibada za binasfi mambo ya msingi ya kuzingatia katika utendaji wa Ibada binafsi ni pamoja na ;-

1.       Mahali pa Ibada
     Mahali pa kufanyia ibada ni muhimu sana kwa mtu anayetaka kuwa na ibada binafsi kwani kama ilivyo kwa ibada nyinginezo kufanyia katika mazingira ambapo familia iko karibu nawewe kunaweza kuifanya ibada hiyo kuingiliwa na mambo mengine  na hivyo kuharibu usikivu unaohitajika kwa hiyo wapi pa kuabudu mara nyingi huchaguliwa na muhusika kulingana na maeneo husika kama ni nyumbani,Kazini ak katika jamii wengine hujibanza katika kona ya chumba na kukutana na Mungu hapo  na usomaji wa Biblia unaweza kufanyika katika meza, baadhi ya wakristo huamua kwenda kanisani kwa malengo hayohayo ya Ibada binafsi, wengine wanavyo vyumba maalumu kwa ajili ya maombi, wengine hufanyia maombi yao makazini wakati wa mapumziko ya chai au chakula wao huyatumia kwa maombi mahali pa utulivu, au wengine nyumbani wakati watoto wanapokuwa wamekwenda shule na wengine kama kina mama hata jikoni  vyovyote iwavyo jambo la msingi ni kupata eneo zuri lenye utulivu litakalokupa mtazamo wa kuweza  kuabudu Binafsi

2.       Muda wa inada Binafsi
     Hakuna muda maalumu wa kuamua kufanya ibada binafsi kwani unaweza kuwa katika kuabudu Binafsi na kuwa katika uhusiano wa kimaombi na Mungu kila wakati hata hivyo inashauriwa na washauri wa kiroho kuwa na wakati maalumu wa kuomba au kuwa na ibada binafsi ingawa biblia inasema ombeni bila kukoma lakini ni muhimu kuwa na namna muda maalumu wa kufanya ibada binafsi  ingawa nmna gani utapanga muda inategemea au inaachwa katika uwezo wa mwabudu mwenyewe kwani ni yeye anayeyajua mazingira yake wengine wana nafasi asubuhi, wengine jioni au wengine hutumia muda wa kuelekea kulala kwa ajili ya ibada binafsi ingawaje asubuhi unaweza kuwa wakati mzuri wa kuanza na Mungu na jioni unaweza kuwa wakati mzuri wa kujichunguza na kumshukuru Mungu kwa uongozi wake wa kutwa nzima na Baraka zake  kwa hiyo haijalishi ni Muda gani vyovyote iwavyo lakini ni vema kuanza na Mungu na kumaliza na Mungu

3.       Namna ya kuabudu binafsi.
     Tunaabudu vipi je tunapiga magoti au tunakaa au tunasimama ni maswali ya msingi lakini jibu moja haliwezi kumtosheleza kila mmoja kanuni kubwa nay a msingi ni kuabudu  katika namna ambayo itakuwa nyepesi kwako  na yenye kukufanya ufurahie  na unayoiona kuwa inatoa heshima kwa mungu na kuonyesha unyenyekevu na heshima  kwa msingi huo wengine hupenda kupiga magoti  wanapoomba au kusoma Biblia  wengine wanakuwa wameketi kimya na wachache hupenda kusimama  jambo la msingi mkao huo ukupe tu muda wa kutosha kuweza kutimiliza ibada yako binafsi uliyoikusudis kuifanya 

4.       Ibada yenyewe inakuaje?
     Wengi wanaweza kuuliza maswali kama ni utaratibu gani unaweza kufuatwa na ni kitu gani kitumike kwa ajili ya ibada ya binafsi hapa pia funguo kuu ni kila mmoja yuko hurukufanya apendavyo katika ibada binafsi  ingawaje matukio Fulani yatakuwa ni ya kawaida kama ilivyo katika ibada nyinginezo kwa msingi huo ili mtu aweze kuabudu Binafsi aweza kuimba wimbo wa kuabudu au tenzi za Rohoni kwa ajili ya kujiandaa na kuyapeleka mawazo yake kwa Mungu , wengine huanza kwa kujisomea neno la Mungu katika kifungu Fulani anachochagua cha kibiblia au kutumia kalenda za usomaji wa Biblia kila siku  baadaya anaingia katika kuomba  maombi yanaweza kuwa ya aina yoyote katika aina zile za maombi tulizojifunza kuhimidi,kushukuru,dua, kuombea wengine, au vyinginevyo kama Roho wa Mungu anavyokuongoza au moyo wako upendavyo, katika ibada Binafsi maombi ya kumuabudu Mungu yaani kuhimidi ni ya muhimu sana , kujitoa pamoja na kushukuru hatimaye unaweza kuiombea familia na mahitaji yako binafsi au kuombea shughuli za kikanisa jamaa na marafiki au ndugu aliyerudi nyuma  na kwa mahitaji mengine ya wakristo usomaji wa maandiko unaweza kusaidia katika toba na kujitoa upya kwa Mungu ibada Binafsi ni maombi ya kipekee yasiyoingiliwa na mtu kwa msingi huo kila mmoja na afanya kama anavyojisikia bila kuingiliwa au kupata maelekezo Fulani tabia ya kufanya ibada binafsi hupelekea katika kufungua mlango wa ukuaji kiroho.

Ibada za kifamilia
     Kuabudu kifamilia ni moja ya jambo la muhimu sana katika maisha ya kiriho na kujitoa kwa Mungu kila familia inaweza kuwa na ibada hizi mara kwa mara ibada za namna hii zinasaidia  katika kushirikiana ukuaji wa kiroho na huweza kusababisha badiliko kubwa la jamii kwa viwango vikubwa kama ikizingatiwa 

Ugumu au kikwazo cha ibada za kifamilia
    Ziko familia nyingine ambazo watu ni wafanya kazi na watoto ni wanafunzi na wakati mwingine hurudi kwa muda mmoja kila mtu akiwa amechoka kwa sababu ya shughuli mbalimbali, na kutokana na shughuli mbalimbali ulimwenguni kunaweza kukaweko na ugumu Fulani katika utekelezaji wa ibada hizi ingawaje zamani ibada za kifamilia lilikuwa ni jambo la msingi na linalofanyika karibu katika kila familia za wakristo  hata hivyo njia pakee inayoweza kusaidia katika utekelezaji wa ibada hizi ni mipango, Ibada hizi huzikutanisha familia pamoja na wote kwa unyenyekevu hukaa pamoja na kuungana katika kumuabudu Mungu kwa pamoja na kujenga imani moja na roho moja Ayubu mtumishi wa Mungu alikuwa hodari kama kuhani wa kuingilia kati na kiongozi wa ibada kwa ajili ya familia yake Ayubu 1;5. Ibada hizi hupanda kitu katika mioyo ya watoto na kuandaa kizazi kijacho kuweza kupokea roho na moyo wa uchaji Mungu mara nyingi katika ibada hizi wanafamilia huimba nyimbo na kasha Baba au mama husoma neno la Mungu  kisha wanafamilia hutoa mchango wao namna walivyolielewa neno  kisha wote huingia katika maombi ibada za kifamilia zinaweza kuchukua Muda wa Nusu saa tu familia zinazofanya ibada za pamoja hujenga uwanja mzuri wa ukuaji wa kiroho na kujenga umoja wa kifamilia ibada za kifamilia zinaweza pia kufanyika katika matukio kama haya yafuatayo

a.       Chakula cha pamoja – wanafamilia wanweza kufanya ibada yao muda mfupi kabla ya kula chakula maarufu kama chakula cha neema
b.      Mna weza kufanya ibada za kifamilia kwa wiki mara moja  kama endapo ratiba zenu zinzkuwa zimebana na hivyo siku kama za mwisho wa wiki ni nzuri kwa ajili ya ibada ya pamoja hii inaweka heshima kwa wanafamilia kuweza kuheshimu ule muda unaokusudiwa kwa ibada ya pamoja
c.       Mna weza kutumia pia tukio kubwa kama sehemu ya kuabudu pamoja matukio haya ni kama vile anapozaliwa mtoto, harusi sikukuu za kukumbuka kuzaliwa  na matukio mengine yanayoweza kuikutanisha familia pamoja kwa kusudi la kuabudu
d.      Wakati wa magumu -  kama familia inapitia mambo magumu mfano tatizo la kifedha , magonjwa  mijadala ya kifamilia basi muda kama huo unaweza kutumika kwa ajili ya ibada ya pamoja
e.      Nyakati za kufanya uamuzi – inapotokea wakati wa kufanya maamuzi Fulani ya kifamilia kam shamba liuzwe au lisiuzwe n.k. pia familia inapokutana kwa hali kamqa hizo watu wanaweza kufanya ibada
f.        Kila jumapili – hii ni ibada ambayo inaweza kufanyika kila jumapili jioni kabisa au usiku tifauti na ibada za kanisani ibada za pamoja kifamilia zina faida kubwa sana na zinajenga umoja  nakuleta nguvu hususani wakati wa mambo magumu vyovyote itakavyo fanyika kwa wakati wowote ukweli unabaki kuwa ibada za kifamilia ni muhimu na zina msaada mkubwa sana Bwana ampe neema kila mmoja kuwa na uwezo wa kuzufanya ibada hizi.
Faida za kuabudu pamoja
     Moja ya faida kubwa ya kuabudu pamoja ni kupata neema ya kuifanya familia iwe na ukristo uliofunzwa kivitendo kuliko kwa maneno hii itawafunza watoto wawe na ujuzi wa kuabudu  zaidi ya ule wanaoupata kwa kuabudu pamoja kanisani  ibada inakuwa ni sehemu ya asili ya maisha ya familia aidha matatizo ya kifamilia yanatatuliwa lupitia maandiko mnayojifunza nyumbani watu wanajifunza kumtumaini na kumtegemea Mungu ,familia inamuona Mungu akihusika moja kwa moja na maisha yao kupitia kujibiwa kwa maombi yanayoombwa pamoja kiufamilia, kunakuwa na ugumu kwa wanafamilia kuiacha imani , watu watajadili maswala ya kifamilia katika mtazamo wa Kikristo inakuwa ni njia ya kupandikiza imani kwa watoto kwa msingi huo basi ni muhimu kwa wazazi kuwa na ujuzi wa kutosha kuhusu Mungu na Neno la Mungu ili kuwarithisha watoto imani iliyo sahii hii itawafanya watoto kuwa wema.
Kuabudu kwa kikundi au makanisa ya nyumbani
   Mtindo huu hauna tofauti na ibada za kifamilia isipokuwa tofauti ni kuwa hapa sasa mnakutana aidha kundi Fulani au wana mtaa Fulani kwa kusudi la kumuabudu Mungu pamoja ibada hizi ni muhimu pia kwa ajili ya kuifikisha injili kwa wengine ibada za vikundi zinaweza labada kukutanisha wafanyakazi wa eneo Fulani au wafanya biashara au wanafunzi walioko mbali na kanisa au nyumbani hizi nazo ni ibada njema na zenye mafanikio makubwa sana ya kuwalea na kuwasaidia katika makuzi ya kiroho.
SURA YA KUMI NA MOJA KUABUDU KATIKA MAISHA
     Mara nyingi sana inasisitizwa kuwa makini na ibada za sdanamu kuna jaribu wakati wote la kujaribu kuabudu vilivyoumbwa kuliko muumba  wakati mwingine inaweza kuwa sio rahisi kugundua kuwa umeabudu sananmu lakini unaweza kujikuta unaabudu bila kujua  ibada inapokuwa haina matokeo yenye kuwafanya watu kubadilika au wakristo kuishi maisha ya ushindi ndipo inapotokea kuwa hata kama hakuna sanamu ya kuonekana kwa macho basin tayari ibada ya sanamu inakuwa imechukua nafasi ibada yoyote ya kweli ni lazima iwe na matunda
1.       Lazima watu wamuhisi Mungu
     Kila watu wanapokuwa wamekutana na Mungu kunakuwa na badiliko jipya linalochukua nafasi kunakuwa na athari ya kiungu kila wakati muamini anapokuwa amekutana na Mungu, maisha yanakuwa ni yenye kutiririka kwa uhusiano na Mungu Mungu hawi wa jumapili tu bali anakuwa ni wa mtu huyo siku zote  Mungu anakuweko kazini shuleni na kila mahali mtu anakokwenda
2.       Kuabudu kwa Ghafla
     Inapotokea kuwa watu wamemuhisi Mungu na kujenga uhusiano naye na kuwa na tabia endelevu ya kuabudu asubuhi na jioni kuna uwezekano wa kutokea nafasi za ghafla za kuabudu  ambazo huweza kusababishwa na Mungu mwenyewe kwa kadiri mwamini anavyokuwa makini katika kuutunza uwepo wa Mungu maishani mwake  hii inaweza kutokea hata wakati wa mambo magumu
3.       Utumiaji mzuri wa mali na vyeo na muda
     Kadiri mtu anavyokuwa na uhusiano mzuri na Mungu katika maisha pia anajikuta kuwa anawajibika katika kila eneo la maisha kuwa kama wakili wa Mungu akitambua kuwa Mungu Mungu amempa dhamana ya kila kitu ikiwemo muda, cheo na mali tulizo nazo tunajiona kuwa tunawajibika kwa kila kitu katika Mungu hii ndio maana Taifa linalomcha Mungu hufanikiwa katika kila eneo ikiwemo utendaji bora aidha waamini watatoa zaka kwa uaminifu na kupenda watu wote bila ya ubaguzi mtu akijitoa kwanza kwa Mungu ndipo anapokuwa na nafasi ya kujitoa nay eye mwenyewe 2Koritho 12;14
4.       Utumiaji wa Mudaau kuukomboa wakati
     Mwabudu wa kweli siku zote atatoa wakati wake kwa Mungu Muda ni maisha na unapozungumzia kuabudu maana yake unazungumzia kutoa muda kwa ajili ya Mungu hii ni gharama  na ndio maana mtume anatoa mwito wa kuukomboa wakati Efeso 5;16 Muda ni maisha na kama maisha yanatolewa kwa mungu maana yake lazima uutoe muda wako kwa hivyo mwabudu wa kweli atakuwa na wakati wa kuokoa muda apate nafasi ya kujitoa kwa Mungu muda utakuwa kitu cha maana kwake
5.       Kumtumikia Mungu
     Kwa asili muitikio wa kuabudu katika roho na kweli hujumuisha pamoja na kumtumikia Mungu kwa sababu kadiri unavyomuabudu mungu kunazaliwa kiu au shauku ya kutaka kuibebe bendera yake yaani kumtumikia  Warumi 12;11, wote kama wanafunzi wa biblia tutakuwa tunafahamu kuwa Isaya alipata witowa kumtumiukia Mungu akiwa hekaluni yaani katika Ibada  na  kama mwitikio wake katika kuabudu alisema ndio nitume mimi bwana Isaya 6;8 Yesu alimuuliza Simeon je wanipenda  kama unanipenda basi lisha kondoo zangu kumbe kumpenda kwetu Mungu kunaweza kuhitimika katika kujitoa kwa kweli na kumtumikia Yohana 21. Nitengeeni barnaba na sauli kwa kazi ile niliyowaitia ni maneno ya Roho Mtakatifu kwa watu waliokuwa wakimuabudu huko antiokia Matendo 13;1-3.
6.       Kujitambua kama mwana wa Mungu
     Kadiri tunavyomuabudu Mungu kama baba hatuwezi kuepuka ukweli wa utambuzi kuwa sisi ni watoto wa Mungu na watoto wa baba mmoja hii inatuunganisha na wana wa Mungu wengine duniani na inaua ubaguzi wa kila aina kadiri unavyoabudu na kuona Baraka za Mungu zikimmiminikia kila mtu ndivyo unavyoweza kutambua kuwa Mungu hana upendeleo Matendo 10 ; 34-35 tutajitambua kuwa wote ni warithi wa Mungu
7.       Kuendelea kuwa watakatifu
     Kadiri mtu anavyokuwa mwabudu ndivyo anavyopata utambuzi wa kuwa anahitaji kujitoa zaidi ndio kwani tunamuabudu Mungu aliyemtakatifu Isaya 6; 1,5. Mtu anapomkaribia Mungu hujiona kuwa na mapungufu hupata nafasi ya kujichunguza Isaya alisema ole wangu na kupata neema ya kutakaswa Biblia inatuamuru kuwa watakatifu hakuna namna yoyote ile inayoweza kutusaidia kuishi maisha matakatifu kama sio Ibada 1Petro 1; 15 Efeso 4;1
8.       Kushuhudia wengine
     Kuabudu wakati wote husababisha ushuhuda kwa wengine kwani kushuhudia, kunatukumbusha tendo la Mungu la kumkomboa mwanadamu kwa niaba yetu hii inatokea pale mwana wa Mungu anapokuwa ameacha dhambi na kujitoa na kujitakasa huweza kupata naffasi ya kubadilika kitabia na mwenendo na kuwafundisha wakosaji zaburi 51;9,13 na kule kuabudu kunatupa msukumo wa kujali wengine na kuwashuhudia injili Matendo 1;8
9.       Kuishi kwa matumaini
Kuabudu kunaqmpa muamini uhakika kuwa ataishi milele ni wazi au bayana kuwa kuna uzima wa milele au kuna maisha baada ya kufa  na kuwa Yesu ndio ufufuo na uzima Yohana 11;25-26, 14;2-3 10;28 kadiri mtu anavyomuamini Mungu aliye hai ndani yake kunakuweko tumaini lililo hai ya kuwa ataishi milele hata baada ya juondoka ulimwenguni pia wanaobaki hawasikitishwi na maisha maovu uliyoishi duniani watasikitika kuwa umejitenga mbali nao lakini watakuwa na uhakika kuwa uko mahali salama kwa sababu ulikuwa mcha Munguhebu basu tujijengee mazoea ya kumuabudu Mungu wetu ili tuwe na tumainai lililo bora Zaburi 95;6-7
SURA YA KUMI NA MBILI WAJIBU WA KIONGOZI WA IBADA
     Yesu kristo alichagua viongozi ambao aliamini kuwa watakuwa msaada kwa waamini wengine kwa ajili ya kuawaidia katika kuwafundisha na kuwasaidia katika ukuaji wa kiroho na maswala ya kuabudu Ni yeye (Yesu) anayetoa wengine kuwa mitume na wengine kuwa manabii na wengine kuwa wainjilisti na wengine kuwa wachungaji na waalimu kwa kusudi la kuukamilisha mwli wa kristo Efeso 4; 11-16.katika kifungu hiki tunajifunza mambo ya msingi nay a muhimu kwa viongozi wa kiroho na wajibu walio nao
1.       Kwamba viongozi wa kiroho yaani mitume manabii wainjilisti wachungaji na waalimu ni zawadi inayotolewa na Mungu kwa kanisa
2.       Viongozi hawa ndio wanaoandaa watu kwa ajili ya kazi ya huduma
a.       Kuujenga mwili wa Kristo
b.      Kufikisha watu kwenye umoja wa imani na maarifa ya kumjua kristo
c.       Kuwafanya watu wawe kama Kristo
Kwa msingi huo utaweza kuona kuwa wajibu huu ni mkubwa na hakuna mwanadamu wa kawaidia anayeweza kuutimiza pasipo msaada wa Roho Mtakakatifu kumbuka kuwa viongozi hawa ndio kichwa kwa mwili wa Kristo hapa simaanishi ile maana ya kuchukua nafasi ya Kristo kama kiongozi mkuu wa kanisa bali nazungumzia ile hali ya viungo vya mwili basi viongozi ni kichwamaisha ya waumini au kundi la mahali pamoja linategemea sana na aina ya kiongozi waliye naye wote tunafahamu kuwa kuna aina nyingi za uongozi lakini ziko aina tatu za uongozi
1.       Viongozi wa imla Authoritarian leader – hawa ni viongozi ambao katika maongozi yao hakuna mtu mwingine anaweza kufanya jambo mpaka yeye aseme ni wenye amri na kuamrisha yeye ndiye mamlaka ya mwisho
2.       Kiongozi huria au ruksa Pamissive leader – Huyu ni kiongozi ambaye huliacha kundi liamue ni namna gani linaweza kuendesha mambo na kuamua kila kitu huyu ni ruksa
3.       Kiongozi mshiriki Participatory leader – huyu ni kiongoshi wa kidemokrasia aanahamashisha lakini anashiriki anaongoza kwa kuwaacha watu huru lakini anasimamia utaratribu uweze kufuatwa
Viongozi ambao wamechaguliwa na Mungu wanajitoa kwaa jili ya maswala ya kiungu na kluwajibika kwa kila jambo katika kuhakikisha kuwa ibada zinafanyika sawa na mapenzi ya Mungu kwa msingi huo tunasema kuwa wachungaji ndio viongozi wakuu wa ibada lakini kwa bahati mbaya wengi wao hawafikiri kuwa wao ni viongozi wa ibada  Mtu moja aliwauliza swali baadhi ya wachungaji vyuoni kuwa ni kazi gani ambayo ni wajibu wenu  wengi walisema kuwa wao ni wachungaji na majibu machache tu yalijibu kuwa wao ni viongozi wa ibada hii ni jambo la kushangaza kwani wachungaji wengi hawajujui kuwa wao ni viongozi wa ibada na hivyo wanashindwa kuwa na Muda wa kupanga namna ya kuendesha ibada  wanachukua Muda mwingi kujiandaa kwa ajili ya jumbe lakini hawachukui muda kuandaa mpangilio mzima wa ibada
     Viongozi wa ibada ni makuhani na ni manabii huiandaa mioyo ya watu na kuhakikisha kuwa inapatana na Mungu lakini pia husema kwa niaba ya Mungu ujumbe wake kwa watu wake
SURA YA KUMI NA TATU VIZUIZI VYA KUABUDU
     Wakati bwana Yesu alipokuwa akiwafundisha wanafunzi wake kusali alisema Bali wewe usalipo ingia katika chumba chako cha ndani na ukiisha kufunga mlango usali mbele za Baba yako aliye sirini na baba yako aonaye sirini atakujazi Mathayo 6;6, Mungu hapendezwi na unafiki anataka watu wamuabudu kwelikweli lakini kuna uwezekano wakati mwingine pasipo kuelewa tukajikuta katika ibada za aina hiyo kwa sababu ya vizuizi mbalimbali vya kuabudi miongoni mwa vizuizi hivyo ni pamoja na
1.       Kusudi la shetani
Mpango mkuu wa shetani ni kuharibu kabisa makusudi ya Mungu na kwa namna Fulani huweza kuwatumia hata wakristo wenyewe kuytimiza mpango wake ,Paulo mtume alitahadharisha kuwa shetani angejaribu kuwaharibu washirika wa Koritho kwa namna ya kuwadanganya , mpango wake ni kuhakikisha kuwa ana harivbu kabisa makusudi ya ibada yenye kumuelekea Mungu 2Koritho 11;3 “Lakini nachelea kama Yule nyoka alivyomdanganya Hawa kwa hila yake, asije akawaharibu fikira zenu, mkauacha unyofu na usafi wa Kristo” Moja ya njia ambayo shetani huitumia katika kuharibu mpango wa Mungu ni kuleta mafarakano na kuleta hali ya kuchanganya shetani alifanikiwa kumtia hawa mashaka kwa kumfanya aamini katika uongo wake uliokuwa unaonekana kama kweli kisha kuanza kuwekea mashaka kweli ya Neno la Mungu akili zetu ndio uwanja wa vita kati yetu na ibilisi tukianza kumsikiliza yeye badala ya Mungu basi taratibi tunaanza kuingia katika mtego Mwanzo 3;1-13. Shetani atatupinga kwa kutumia tama zetu na kwa sababu hiyo itatupasa kumpinga 1Petro 5;8-9, atatumia hisia zetu hali za kujiona kuwa hatufai, wivu, faraka , masengenyo, na kutukatisha tama ili yamkini kwamba tuweze kuondoa mawazo yetu katika Mungu,atatumia hali zetu za kuchoka na kutusumbua kwa shida ambazo tutaanza kuziangalia hizo na kuacha kumuangalia Mungu atatumia watu wanaopagawa na pepo kuharibu hali ya kuabudu na watu wanaochelewa ibada ambao watatliza viatu vyao ili kutoa usikivu wa watu kutoka katika kuabudu na kumwangalia aliyechelewa, hata hivyo tiukumbuke kuwa nguvu zake zina mipaka na kuwa tukimuomba Mungu tunaweza kumshinda
2.       Kuipenda Dunia
Ni muhimu kufahamu kuwa shetani anaweza kutumua pia hali za kukuvuta kimawazo kutoka katika kufikiri maswala ya ibada na kuanza kufikiri maswala ya kidunia hili si jambo la ajabiu si unakumbuka mkewe Lutu hata akatika hali ya ibada ya kuokolewa na kuhukumiwa kwa sodoma yeye bado alikuwa akiipenda Sodoma na hakuweko na tendo la kuokolewa kwawe halikuwa na maana, wakati wa ibada sio wakati wa kufikiri watoto watakula nini, wapi utafanya shoping au mkeo yukoje au kuruhusu mawazo ya kidunia tama na uasherti kutembea katika akili zetu 1Timotheo 5;8, ni kweli Mungu ametutaka tuzijali familia zetu lakini kuwaza wapi utapata fedha na kuitunza familia yako wakati wa ibada sio sahii 1Timotheo 6;10 utafuteni kwanza ufalme wa Mungu na haki yake na mengine yote mtazidishiwa1Yohana 2;15-17
3.       Tabia mbaya sizizofaa.
Hali yoyote ya maisha ya dhambi za mtu binafsi, kutokuomba na tabia zisizofaa ni kizuizi kikubwa kwa ibada ni muhimu kufahamu kuwa Paulo mtume aliwataka waamini kuwekqa mbali kabisa matendo ya mwili Warumi 7-8, 1Koritho 3;1-4 aina zozote za matengano na faraka na kutokuelewana ni kizuizi kwa ibada , mtu awaye yote akitaka kumfuata Yesu anatakiwa kujikana nafsi na kumfuata Mathayo 16;24,Marko 8;34 na Luka9;23, aidha matendo yoyote yasiyotokana na utii husababisha kikwazo kwa ibada sauli alishindwa kutii na alijikuta anakataliwa 1samuel 13;11-14 dhambi na mambo mengineyo mengi huweza kuwa kizuizi cha ibada
4.       Mtazamo mbaya
Wako watu ambao mtazamo wao sio mzuri sana katika maswala ya kuabudu wana hali ya kukosoa kila kitu, wana uchungu na hawataki kusamehe, na huwa na kiburi, hali kama hizo ni kizuizi kwa ibada soma Yakobo 3; 9-12 inasema hivi
     “Kwa huo twamuhimidi Mungu baba yetu na kwa huo twawalaani wanadamu waliofanywa kwa mfano wa Mungu katika kinywa kilekile kwatoka Baraka na laana …..” watu ambao wanaebdekeza ukosoaji na kupingana na neno la Mungu tayari aikili zao ziko mbali na Mungu aidha awaye yote ambaye anakuja mbele za Mungu huku anajifikiri kuwa ni bora kuliko wengine hawezi kujipatia kibali kwa Mungu Mungu nhuwapinga wenye kiburi bali huwapa neema wanyenyekevu Yakobo 3;2 sisi sote runajikwaa katika mambo mengi na hivyo hakuna mtu mkamilifu hatupaswi kuwa wahukumu wa wengine na kujifikiri kuwa sisi ni bora kuliko wao eti kwa sababu wana udhaifu huu ama ule na sisi kujiona kuwa wenye haki ibada ya kweli lazima isimamie msingi wa kuwa na upendo kwa wengine Mtume Yohana anakazia kuwa huwezi kuwa na madai kuwa unampenda Mungu huku unachukia wengine 1Yohana 3;10, 4;20
5.       Hali ya kutokusamehe
Yesu alifahamu kuwa roho ya kutokusamehe ni kizuizi kikubwa sana cha ibada na kwa sababu hiyo alitoa mafundisho yafuatayo;-
    “Mathayo 5; 22-24 bali mimi nawaambia kila mtu amwoneaye ndugu yake Hasira itampasa hukumu,…..Basi ukileta sadaka yako madhabahuni na huku ukikumbuka ya kuwa ndugu yakko ana neno juu yako iache sadaka yako mbele ya madhabahu uende zako upatane kwanza na ndugu yako…”ukweli ni kwamba hakuna ibada bila kusamehe wala hakuna maombi bila kusamehe wala hakuna toba kusamehewa bila kusamahe wengine kwanza mathayo 6; 12,14-15. Efeso 4;32 Biblia ina sisitiza kusameheana kwanza kama Kristo alivyotusamahe
6.       Uchungu
Hata pale inapotokea kuwa wengine wanaweza kutusababishia machungu ni muhimu kufahamu kuwa uchungu huo utaathiri ibada zetu waandishi wa agano jipya wanaonya habari ya kuwa katika uchungu kuwa si njema Matendo 8;23,Warumi 3;14,Efeso 4;30-31,Waebrania 12;15,Yakobo,3;14
7.       Kiburi
Hali ya kutokusamehe , kuwa na uchungu na roho ya kukosoa kila jambo jema zinatupelekea kupeleka mawazo yetu kwa watu zaidi kuliko kwa Mungu na pia hali ya kujiona kuwa sisi tulistahili jambo Fulani na kwa msingi hio basi inajenga kiburi na kutuondoa katika mpango wa Mungu Yakobo 4;6 “Mungu huwapinga wenye kiburi bali huwapa neema wanyenyekevu” kama wakristo watakuwa na upendo wa kweli basi hali ya kujiona kuwa unafaa itaondoka na tutawapenda wengine upendo haujivuni kiburi sio mfano wa Kristo  ni muhimu kukumbuka kuwa yeye alikuwa yuna namna ya Mungu lakini alikuwa mnyenyekevu sana na mtii Wafilipi 2;5-8 mambo ya aina hii yote huiharibu ibada na kama tutaklazimisha kuabudu huku hatukubali kuyaweka kando mambo hayo ibada hizo zitakuwa hazina faida na tutatimiza mathayo 15; 7-9 unaosema “Enyi wanafiki ni vema alivyotabiri Isaya kwa habari zenu akisema watu hawa huniheshimu kwa midomo ila mioyo yao iko mbali name nao waniabudu Bure wakifundisha mafundisho yaliyo maagizo ya wanadamu” unaona kumbe kuna uwezekano wa watu kuabudu Bure tu yaani kuabudu pasipo faida mpendwa endapo maswala hayo hapo juu yataonekana katika maisha yetu na tukayakubali kututawala basi shetani atakuwa ametushindwa kwa kuwa tumekosa kuzitambua fikra zake
SURA YA KUMI NA NNE NAMNA YA KUWASILISHA IBADA
     Ninapotaka kuzungumzia swala la uwasilishaji ibada nataka nikuonyeshe kwanza stori ya mtumishi mmoja wa Mungu ambaye alikuwa anasheherekea siku yake ya kuzaliwa yaan Birthday mtumishi huyu alikuwa na watoto wanne wote walikuja kumpongeza baba yao na kumpa zawadi wa kwanza ambaye alikuwa na miaka 26 wa kike, alimpa zawadi ya Fedha baba yake kwa ajili ya kutembea kokote atakako kisha akambusu baba yake na kumwangalia kwa upendo, wa pili ambaye alikuwa na miaka 23  wa kike Yeye alichora picha nzuri sana na alimkabidhi baba yake kisha akambusu na kumkumbatia na kumnong’oneza kwa sauti ndogo nakupenda baba, kisha mtoto wa tatu mwenye miaka 21 wa kiume yeye alileta shati zuri kisha akamvalisha baba yake mabegani na kumwambia wewe ni baba wa pekee duniani na wa mwisho mwenye miaka 16 wa kiume alimpa baba yake saa aliyokuwa amenunua safarini na kisha akamwambia Baba yake najivunia kuwa na baba kama wewe bila shaka utaipenda zawadi hii.
      Unajifunza nini katika mfano huu? Kila mtoto anayo namna yake ya kuonyesha upendo na shukurani kwa baba yake na kama ambavyo kila zawadi ilikuwa tofauti hali kadhalika namna walivyoonyesha upendo na maneno waliyoyatoa yalikuwa tofauti je unafikiri kuna aliyempendeza baba yake zaidi kuliko mwingine? Bila shaka hapana wote walimpendeza hivyo ndivyo Mungu anavyopendezwa na kila mtu anayeonyesha upendo wake kwake na kwa msingi huo basi ni muhimu kufahamu kuwa kila ibada kama imeelekezwa kwa Mungu katika hali ya kumpenda basi hata kama ni tofauti na ile uliyoizoea Mungu anapendezwa nayo Najua wako watu wanaweza kufikiri kuwa Ibada zao ni bora kuliko za wengine sikiliza mpendwa kila mtu anayo namna yake ya kuonyesha kuwa anampenda Mungu hivyo basi kama utaishi ulimwenguni humu na kutaka aina Fulani ya ibada uliyoizoea wewe  na kufikia ngazi ya kudharau za wengine tayari umejivuna na unamuhitaji Kristo je hujawahi kuona wakristo wakiruka baadhi ya makanisa ambayo wangeweza kabisa kuabudu hapo labda yako karibu nao kuliko kule wanakoelekea kuabudu lakini kwa sababu ya mazoea utawasikia aha! Ibada za pale sijui zikoje mi sijazizoea haya si mazoea mazuri. Mungu hupendezwa na kila ibada inayotolewa katika misingi ya uwazi, na wepesi, isiyohusisha kujiangalia, yenye kanuni ya upendo, inayotoka moyoni na isiyo ya kinafiki ibada inapozingatia hayo inakuwa imewasilishwa katika njia inayoweza kabisa kumpendeza Mungu na haya ndio tunayoyaangalia hapa tunapozungumzia namna ya kuwasilisha ibada.
1.       Lazima iwe yenye msingi wa uwazi na rahisi.
    Mara nyingi kibinadamu huwa tunaogopa kuona wenzetu watatuonaje na hivyo tunashindwa kujifunua uhalisia wetu kwamba sisi tukoje, Tunahofia kwamba labda wakijua jinsi tulivyo wanaweza kutudharau au kupoteza heshima yetu,na ndipo unapokuta kuwa tunajaribu kuficha hisia zetu, kila binadamu anapenda kukubalika kwa wengine na ndio maana hali hii huathiri hisia zetu waklati tunapokuwa mbele za Mungu katika kuabudu tunajarinbu kubania hisia zetu mtu anaweza kuwa anajisikia kulia lakini akaogopa watu watamuonaje hii inatunyima uhuru na uwazi wa kumuabudu Mungu kwa urahisi , Bila shaka unakumbuka mfano wa mama Yule aliyekuwa akitokwa na Damu kwa muda wa miaka kumi na miwili kwa kuogopa makutano aliamua kwenda kwa siri ili kugusa upindo wa vazi la Yesu na kupokea uponyaji wake Luka 8;47-48 Mtu huyu alimgusa sana Bwana Yesu na Yesu alipohoji kuwa ni nani aliyenigusa kila mtu alijaribu kukanusha lakini Yesu alimwambia imani yako imekuponya tunao watu wengi wa jinsi hii ambao hurudi toka Ibadani wakiwa bado hawajaguswa hisia zao kwa sababu hawako wazi kwa ajili ya kuhudumiwa na Mungu
    Tusikubali kudanganyika kwani kuna wakati itatupasa kuwa wajinga ili tuwe wenye hekima Paulo alitoa ushauri huu 1Koritho 3; 18, 21, 23. Wakati wa kuabudu acha kujibana mwaga hisia zako zote kwa Mungu kwa uwazi na Mungu atakusaidia
    Wakati wa kuabudu kubali kukutana na uso wa Mungu, Yesu alipojifunua kwa Simeon Petro baada ya kufanya muujiza Petro alijiona kuwa mwenye dhambi na kumwambia Ondoka kwangu ee bwana mimi ni mwenye dhambi Luka 5; 8 lakini ujuzi wake kuhusu Mungu ulivyokua unaendelea kukua hatimaye aliendelea kuambatana na bwana Yesu na alikuwa huru na hakujikakamua kuubania kuonyesha utu wake bali hata kuonyesha udhaifu wake kwa Yesu na Mungu hakumfukuza!
     Mwanamke aliyekuwa kahaba alikwenda kumgusa Bwana Yesu Lakini farisayao alikasirishwa na kufikiri kama huyu angekuwa nabii yaani Yesu angejua kuwa mwanamke anayemgusa ni kahaba jinsi gani.Lakini Yesu aliwajua wote yeye alijua mpaka mioyo yao alitambua kuwa mwanamke huyu ni wa namna gani na kuwa mguso wake unahitaji msamaha wa dhambi lakini farisayo hakuwa tayari kufunua hisia zake akijifikiri kuwa yeye ni mwenye haki na huku akiwa hana habari kuwa anatawaliwa na kiburi, Ndugu yangu sikiliza hatuwezi kamwe kumdanganya Mungu kuhusu jinsi tulivyo yeye anatujua na  kumuabudu kwetu kwa namna ya kinafiki kunatupelekea kutokumgusa lazima tutubu dhambi zetu na kukubali kuachilia wazi hisia zetu kwa uwazi kwa Mungu na kwa urahisi
2.       Lazima iwe isiyohusisha kujiangalia yaani kujiachia uwe huru
Tumeona mara kadhaa watu wakimjia Mungu kwa sababu ya shida za ndani kabisa sifikiri kama kuna ubaya kwa hilo hata pale moyo wako unapokuwa umeumizwa bado unaweza kuja kwa Mungu na kumueleza hisia zako majaribu yetu hutuleta karibu na Mungu na wakati mwingine hutusaidia kutufanya tukomae kiroho Yakobo 1;2-4 zaburi nyingi zinaonyesha hisia za watu waliopitia mateso ya aina mbalimbali lakini yaliwaleta karibu na Mungu,Jambo la msingi ni kukubali kujiachia na kutokujiangalia tunapokuja kwa Mungu katika ibada  tuwe huru kuweka wazi hisia zetu na kujisahau tukiabudu na kumsifu na kumtukuza kwa moyo
3.       Lazima kuwe kwa kanuni ya Upendo
     Mathayo 22;27-29 Amri kuu ni Upendo kumpenda Mungu na kuwapenda jirani zetu, Tunamuabudu Mungu kwa sababu tunampenda tunaimba nyimbo kwa sababu tunampenda tunapokuwa na wenzetu katika makundi tunarudia tena na tena kuonyesha kuwa tunampenda Mungu, zaidi ya yote tunapoishi maisha yenye kuonyesha kumpendeza Mungu au maisha ambayo Mungu anakusudia tuyaishi ni kuonyesha wazi kivitendo namna tunavyompenda Mungu na lolote tulifanyalo tunalifanya kwa sababu tunampenda Mungu namna hii ibada inakuwa katika kanuni ya kufanya kila kitu kwa upendo na sio sheria, Hata hivyo kumpenda kwetu Mungu hakuwezi kuwa kamili kama tutakuwa hatuwapendi ndugu 1Yohana 3;14 upendo wetu kwa wengine unafunuliwa kama vile tuwapendavyo wana familia zetu,jambo hilin litatufanya tumuhudumie kila mtu na kuwatumikia wote na kuwalinda wasikwazike au kuumizwa moyo na kuwasaidia wote katika ukuaji wa Kiroho Mathayo 25;34-46.Paulo alimuamuru Filemoni kuonyesha pendo kama hili kwa Onesmo Filimon 4-7. Upendo unapokuwa ndio kanuni ya ibada uhusiano na Mungu utakuwa wenye kudumu katika kusanyiko la ibada hivyo ni muhimu kukazia kanuni ya upendo katika kusanyiko lolote lile ambalo linakusudia kumpendeza Mungu na kutaka kuutunza uhusiano wao na Mungu Uwepo wa Mungu leo unaondoka makanisani au haupo kabisa kwa sababu nyingi lakini mojawapo ni hii ya kupuuzia upendo makanisani sasa kuna chuki,migawanyiko, kukosekana kwa amani upendeleo na hata ile tabia ya samaki mkubwa kumeza mdogo,tajiri kuendelea kuwa tajiri na masikini kuwa maiskini hizi ni hali halisi kwa makanisa yaliyofanikiwa kifedha huko mjini kuyasahau makanisa masikini ya vijijini bila shaka hilo nalo ni neno kivitendo! Ndani ya washirika na watumishi leo hakuna kuvumiliana, kuna kuchukuliana hatua kwa haraka, kuna wivu, kuna tabia mbaya zisizo za kimaadili, hakuna utu wema, hakuna uaminifu,hakuna kulindana, kila mtu anaonyesha umwamba, hakuna kusaidiana, hakuna huduma ya kurejeshana, watu wana hasira za haraka, watu wanahukumiana, wala hawajali na hawataki kukiri kuwa wamekosea, wanteteana kukandamiza wanyonge, wanaiba sadaka n.k hii yote ni kwa sababu upedno wa kweli umetoweka leo mahali pa jinsi hiyo ibada haiwezi kuwasilishwa vema
4.       Lazima iwasilishwe pasipo unafiki
Yesu alikuwa akifundisha juu ya ibada ya kweli na ibada ya kinafiki alitoa mfano huo kuonyesha ni ainagani ya ibada inakubalika kwa Mungu Luka 18;10-14 Biblia mahali hapo inasema
     Watu wawili walipanda kwenda hekaluni kusali,mmoja farisayo,wa pili mtoza ushuru ,Yule Farisayo akasimama akiomba  hivi moyoni mwake Ee;Mungu nakushukuru kwakuwa mimi si kama watu wengin , wanyang’anyi,wadhalimu, wazinzi, wala kama huyu mtoza ushuru, Mimim nafunga mara mbili kwa juma,hutoa zaka katika mapato yangu yote.Lakini Yule mtosha ushuru alisimama mbali wala hakuthubutu hata kuinua macho yake mbinguni, bali alijipiga piga  kifua akisema Ee;Mungu uniwie radhi mimi mwenye dhambi
Farisayo alifanya kosa kubwa sana hakua anaabudu kabisa ibada ya kweli, wala hakumpa Mungu utukufu na badala yake alikuwa akijitukuza mwenyewe alikuwa amejaa kiburi na majivuno eti kwa sababu hakuwa mwenye kudhulumu wala mnyang’anyi, mzinzi au mtoza ushuru, alijivunia swala la kufunga na kutoa zaka, kama kweli haya aliyoyasema farisayo ni kweli na kuwa alikuwa akiyyafanya vyovyote iwavyo Ibada yake ilikataliwa wala haikukubalika haya hayakuwa maombi bali yalikuwa ni majivuna hii haikuwa ibada je hujawahi kuona wewe wahubiri wakijua wazi kanbisa mahubiri ni sehemu ya ibada lakini wakiyatumia kuponda wengine na kujisifu wakieleza mafanikio waliyo nayo na wake wazuri waliopewa na kuwaponda wale wanaowaita kuwa wanajidai huku hawana kitu chochote cha ziada au kufumbia watu mafumbo na mahubiri yamekuwa kama mipasho ya taarabu hayana hata chembe ya utukufu kwa Mungu? Muda usingeliweza kutosha kukukonyesha jinsi waimbaji wanaoitwa wa injili wakiimba katika nyimbo zao kama watu ambao nyimbo zao hazimpi Mungu utukufu na badala yake zinajibizana na hali halisi ya habari zao katika magazeti au kuwasema watu wa mahali Fulani , waiume zao, wanamuziki wenzao, na hakuna tofauti na ile mipasho ya taarabu, fuatilia hata mahubiri katika televisheni leo utaweza tu kujua kuwa wahubiri hao wanapondana na wameacha kusudi la kuwafikia watu na kuwakutanisha na Mungu sasa wanasagiana Je haya ndio makusudi ya kuhubiri katika vyombo vya habari, fuatilia katika magazetiya Kikristo leo  je yanatoa mafundisho au yamejaa sera za kujipigia debe ili waendelee kuchaguliwa kwa mara ya kadhaa kuwa viongozi wakubwa wa makanisa yao hayo yote yanatukumbusha kila alichokifanya Yule farisayo ibada yake ilikataliwa
   Ni muhimu ikumbukwe kuwa Yesu alitoa mfano huu kutukumbusha juu ya watu ambao wanafikiri kuwa wana uhakika na yale wanayoyafanya kama kwamba ni mapenzi ya Mungu hawa ni watu waliojikinai wenye kujihesabia haki Luka 18;9, Isaya 64;6 Biblia inasema hivi katika Isaya 64;6 “Kwa maana sisi sote tumekuwa kama mtu aliye mchafu,na matendo yetu yote ya haki yamekuwa kama nguo iliyotiwa unajisi,sisi sote twanyauka  kama jani na maovu yetu  yatuondoa kama upepo uondoavyo”Hakuna hata mtu mmoja awezaye kusimama mbele za Mungu akiwa salama au anastahili je wewe unastahili mbele za Mungu? Kumbuka ni kwa neema yake tu tunaweza kumkaribia wala si kwa haki zetuTito 3;4-5 inasema hivi Lakini wema wake Mwokozi wetuMungu na upendo wake kwa wanadamu ulipofunuliwa alituokoa si kwa sababu ya matendo ya haki tuliyoyatenda sisi bali kwa rehema yake kwa kuoshwa kwa kuzaliwa kwa pili na kufanywa upya na Roho Mtakatifu unaona! Kumbe wokovu ni kazi ya Mungu, kukubalika kwetu kwake ni kazi yake hatuna cha kujisifia Hubiri kwa unyenyekevu,imba kwa unyenyekevu abudu kwa unyenyekevu fanya kwa moyo mkunjufu nauliopondeka na kwa upendo ndugu hakikisha ibada yako inapata kibali mbele za Mungu kuabudu katika Roho na kweli ni rahisi lakini sio rahisi kwa watu wanaojifikiri kuwa bora kuliko wengine. Endapo eneo hili limekugusa ndugu msomaji wangu shirikiana name katika sala hii

“Mungu mwema ni wewe ninayetaka kukutukuza, wala sio wengine wala sio mimi mwenyewe, wewe pekee ndiye unayestahili sifa zangu, ninapokuja kwako kumwaga hisia zangu nisaidie kujisahau na kukuangalia wewe ili kwamba matatizo yangu na mizigo yangu isinizuie kukuona,Nifanye kuwa huru na kukupenda na Roho wa Mungu anisaidie kuwa huru na kuniongoza ili nikuabudu kwa furaha,Nifanye kuwa mtumwa wa wengine ninapokuabudu,lifanye pedno kuwa kanuni yangu ya ibada nikupende wewe na watu wotena nikuabudu wewe kwa unyenyekevu na kuvunjika nisihukumu wengine bali nikuletee wewe heshima na utukufu kwa ajili ya jina lako takatifu amen!
SURA YA KUMI NA TANO:  KUABUDU HUKO MBINGUNI
Ibada iliyokamilika
     Hakuna ibada iliyokamilika kwa sababu wanaoabudu pia hawajakamilika ni huko mbinguni ndiko kutakuwa na ibada iliyokamilika kabisa, moja ya mambo yanayotufanya tuwe na ibada isiyo kamilika ni kwasababu hatuwezi kuyafahamu mambo ya Rohoni mpaka Roho wa Mungu aweze kutufunulia na ingawaje anaiganya kazi ya kutufunulia lakini ni kwa sehemu, Mungu yuko katika ngazi ya juu sana kuliko tulivyo wanadamu sisi tuna mipaka karibu katika kila eneo la maisha lakini kule mbinguni ufahamu wetu utaongezeka na tutafahamu kwa ukubwa zaidi machoyetu na fahamu zetu zitafunguliwa kwa upana zaidi na maswala ya kiroho yatakuwa dhahiri kuliko sasa ambao tunaona kwa jinsi ya fumbo na kufahamu kwa sehemu Biblia inasema hivi katika 1Koritho 13;9-12
Kwa maana tunafahamu kwa sehemu na tunafanya unabii kwa sehemu lakini ijapo ile kamili iliyo kwa sehemu itabatilika, Nilipokuwa mtoto mchanga nalifikiri kama mtoto mchanga,tokea hapo nilipokuwa mtu mzima nimeyabatilisha mambo ya kitoto,Maana wakati wasasa tunaona kwa kiookwa jinsi ya fumbo wakati ule nitajua sana kama na mimi ninavyojuliwa sana”
Paulo hapa anazungumzia jinsi atakavyokuwa huko mbinguni hii ndio hali halisi huko tutamwona mwokozi usokwa uso na ufahamu wetu kuhusu Mungu utakamilika huko, sio tu ujuzi kuhusu Mungu lakini hata na sisi wenyewe tutajitambua kwa ukamilifu kwa kuwa kazi njema aliyoianza katika mioyo yetu ataikamilisha Wafilipi 1;6, lini itakuwa hivyo tusubiri maana kwa sasa hakuna ajuaye
Nani wataabudu
Ni wale washindao tu ndio watakaomwabudu Mungu huko mbinguni mkazo wa ushindi unaonekana zaidi katika nyaraka ndani ya kitabu cha ufunuo kwa makanisa yale saba
1.       Ufunuo 2;7 Yeye ashindaye nitampa kula matunda uya mti wa uzima ulio katika biustani ya Mungu
2.       Ufunuo 2;11 Yeye ashindaye hatapatikana na madhara ya mauti ya pili
3.       Ufunuo 2;17 Yeye ashindaye  nitampa baafdhi ya ile mana iliyofichwa name nitampa jiwe jeupe  na juu ya jiwe hilo limeandikwa jina jipya asilolijua mtu ila yeye anayelipokea
4.       Ufunuo 2; 26-28 Yeye ashindaye nitampa mamlaka juu ya mataifa,name nitampa ile nyota ya asubuhi
5.       Ufunuo 3;4-5Yeye ashindaye atavikwa mavazi meupe wala sitalifuta jina lake katika kitabu cha uzima
6.       Ufunuo 3;12 Yeye ashindaye  nitamfanya kuwa nguzo katika hekalu la Mungu wangu
7.       Ufunuo 3;21 Yeye ashindaye nitampa kuketi pamoja nani katika kiti change cha enzi.
Ni furaha ya ajabu kwani hawa washindao Yohana anafunua katika sura ya 7 kuwa ni wengi sana
Ndugu yangu mpendwa zingatia basi maswala ya ibada na uishi maisha ya ushindi ilei wewe na mimi kwa neema ya Mungu tuweze kufikia hatua ya ushindi na kumuabudu Mungu wetu katika kweli iliyokamilika mbingunii Ubarikiwe na Bwana !.
Mkuu wa wajenzi mwenye Hekima!