Jumatatu, 29 Juni 2020

Jinsi ya kushinda vikwazo ulimwenguni!

Yohana 16:33 “Hayo nimewaambieni mpate kuwa na amani ndani yangu. Ulimwenguni mnayo dhiki; lakini jipeni moyo; mimi nimeushinda ulimwengu.



Utangulizi:


Maisha yetu Duniani yamejaa yamejaa milima na mabonde, kila mwanadamu anapozaliwa duniani ni kama ameletwa ili aweze kupambana na changamoto mbalimbali, kuna nyakati za giza na kuna nyakati za nuru, Katika nyakati hizo za changamoto mbalimbali, wengi wetu tunaachwa na maumivu makubwa na mateso ya aina mbalimbali na wakati mwingine tunaweza kupoteza tumaini, wakati mwingine tunaweza kujiuliza hivi kweli Mungu yupo? Na kama yupo anaona haya tunayoyapitia? Tunaweza kujikuta tunakata tamaa na kuvunjiika moyo na  kupoteza imani kwa Mungu!, Kristo Yesu katika Yohana 14-16 alipokuwa anahitimisha safari yake ya kazi duniani alianza kuzungumza maswala kadhaa ynayoashiria dhiki itakayowapata wanafunzi wake neno analolitumia Yesu hapo ni TRIBULATION ambalo maana yake ni mateso, taabu, changamoto au vikwazo vya namna mbalimbali anaonyesha kuwa haya yapo kwa sababu tuko duniani kwa hiyo katika maisha ni lazima tukutane nayo na kuyakabli, kwa msingi huo kama watu wa Mungu hatupaswi kuvunjika moyo kutokana na vikwazo mbalimbali na badala yake hatuna budi kukabiliana navyo kwa imani na kuhakikisha tunatoboa anga jingine katika maisha haya hii ni kwa sababu Yesu ametuhakikishia ushindi siku zote za maisha yetu! Na adui yetu mkuu amekiwsha kushughulikiwa, Yesu sio tu ameushinda ulimwengu lakini pia ametuachia njia ambazo kwa hizo tunaweza kushinda vikwazo vyote! 1Petro 4:12 “Wapenzi, msione kuwa ni ajabu ule msiba ulio kati yenu, unaowapata kama moto ili kuwajaribu, kana kwamba ni kitu kigeni kiwapatacho.    

          
1.        Kumbuka  Hakuna jambo lililo gumu la Kumshinda Mungu

a.       Mwanzo 18:13-14 “BWANA akamwambia Ibrahimu, Mbona Sara amecheka akisema, Mimi kweli nitazaa mwana, nami ni mzee? Kuna neno gani lililo gumu la kumshinda BWANA? Kwa muhula wake nitakurudia, wakati huu huu mwakani, na Sara atapata mwana wa kiume.”  Abraham na Sara walikuwa wakitazamia kupata mtoto na muda mrefu sana ulipita hata wote wakawa wazee Sara akakoma katika siku zake za kawaida ya wanawake Hata Mungu alipowatokea na kuwaahidi kuwa watapata mtoto Sara alicheka sana bila shaka alifikiri inawezekanaje katika uzee kama ule yeye kupata mtoto Mungu alimjibu Abrahamu kuwa Hakuna neno lililo gumu la kumshinda Bwana !


b.      Hesabu 11:21-23 “Musa akasema, Watu hawa ambao mimi ni kati yao, ni watu sita mia elfu waendao kwa miguu; nawe umesema, Nitawapa nyama, ili wale muda wa mwezi mzima.  Je! Makundi ya kondoo na ng'ombe yatachinjwa kwa ajili yao, ili kuwatosha? Au samaki wote wa baharini watakusanywa pamoja kwa ajili yao, ili kuwatosha? Bwana akamwambia Musa, Je! Mkono wa Bwana umepungua urefu wake? Sasa utaona kwamba neno langu litatimizwa kwako, au sivyo.” Mungu alipokuwa amewaokoa wana wa Israel kutoka utumwani kule Misri alianza kuwalisha jangwani kwa chakula maalumu kutoka Mbinguni kiitwacho mana kwa muujiza hata hivyo wana wa Israel walianza kulalamika kuchoshwa na chakula hicho na wakaanza kumdai Musa awape nyama jambo hili lilionekana kama haliwezekani kwa Musa lakini Mungu aliahidi kuwa atauliza mkutano ule kwa nyama tena sio katika siku moja bali mwezi mzima mpaka wazikinai musa aliona kama jambo hili ni jambo lisilowezekana lakini Mungu alimjibu kuwa Hakuna lisilowezekana kwa Mungu!


c.       Yeremia 32:17 “Aa! Bwana MUNGU, tazama, wewe umeziumba mbingu na nchi, kwa uweza wako mkuu na kwa mkono wako ulionyoshwa; hapana neno lililo gumu usiloliweza;” Hakuna jambo lolote lililo gumu asiloliweza Bwana Mungu wetu hivyo tunapokutana na changamoto za aina mbalimbali hatuna budi kuliitia jina la Bwana kwa imani tukijua ya kuwa Mungu wetu anaweza na atatusaidia na kutukomboa na kutupa ushindi katika hali yoyote tunayoipitia wengi tuliomtumaini alitusaidia na kutukomboa na kututoa katika kutazamia kwa adui yetu .


2.       Kumbuka shuhuda zake


Zaburi 124:1-8 “Kama si Bwana aliyekuwa pamoja nasi, Israeli na aseme sasa, Kama si Bwana aliyekuwa pamoja nasi, Wanadamu walipotushambulia. Papo hapo wangalitumeza hai, Hasira yao ilipowaka juu yetu Papo hapo maji yangalitugharikisha, Mto ungalipita juu ya roho zetu; Papo hapo yangalipita juu ya nafsi zetu Maji yafurikayo. Na ahimidiwe Bwana; Asiyetutoa kuwa mawindo kwa meno yao. Nafsi yetu imeokoka kama ndege Katika mtego wa wawindaji, Mtego umevunjika, nasi tumeokoka. Msaada wetu u katika jina la Bwana, Aliyezifanya mbingu na nchi.Mwandishi wa zaburi hii amejaa shuhuda za Bwana anakumbuka matendo makuu ya Mungu na uwezo wake mkuwa wa kuwaokoa Israel anakumbuka hatari zote ambazo wana wa Israel walipitia na anakumbuka mashambulizi yote wana wa Israel waliyapitia jinsi walivyokusudiwa mabaya au kumezwa hai, anakumbuka hasira za adui zilivyokuwa mbaya sana juu yao lakini Mungu aliiokoa nafsi yake na watu wake anakumbuka kuwa Mungu ni msaada, siku zote tunapokabiliana na changamoto yoyote na jambo lolote lilolo gumu kumbuka shuhuda zake shuhuda za ushidi ndio zitakukumbusha kuwa Mungu ni nani na zitakufanya uione changamoto iliyoko mbele yako kuwa ndogo na kuwa itapita pia ona 1Samuel 17:32-37 “Daudi akamwambia Sauli, Asizimie moyo mtu ye yote kwa ajili ya huyu; mimi mtumishi wako nitakwenda kupigana na Mfilisti huyu. Sauli akamwambia Daudi, Huwezi wewe kumwendea Mfilisti huyu upigane naye; maana wewe u kijana tu; na huyu ni mtu wa vita tangu ujana wake.Daudi akamwambia Sauli, Mtumishi wako alikuwa akichunga kondoo za baba yake, na alipokuwa akija simba, au dubu, akamkamata mwana-kondoo wa lile kundi, mimi hutoka nikamfuata, nikampiga, nikampokonya kinywani mwake; na akinirukia, humshika ndevu zake, nikampiga, nikamwua. Mtumishi wako alimwua simba na dubu pia; na huyu Mfilisti asiyetahiriwa atakuwa kama mmoja wao, kwa sababu amewatukana majeshi ya Mungu aliye hai. Daudi akasema, Bwana aliyeniokoa na makucha ya simba, na makucha ya dubu, ataniokoa na mkono wa Mfilisti huyu. Sauli akamwambia Daudi, Enenda, na Bwana atakuwa pamoja nawe.” Shuhuda za matendo makuu ya Mungu ni muhimu kwetu, mkumbuke Mungu alivyokushidnia katika mambo mengi makubwa na magumu na jua kuwa Mungu yuleyule aliyekusaidia katika 1 na 2 na 3 atakusaidia na hili unalokabiliana nalo!


3.       Kumbuka Neno la Mungu.

Waebrania 4:12 “Maana Neno la Mungu li hai, tena lina nguvu, tena lina ukali kuliko upanga uwao wote ukatao kuwili, tena lachoma hata kuzigawanya nafsi na roho, na viungo na mafuta yaliyomo ndani yake; tena li jepesi kuyatambua mawazo na makusudi ya moyo.” Neno la Mungu ni sauti ya Mungu lina mamlaka lina nguvu na ufunguo wa suluhu kubwa na nyingi ya maisha yetu, Hatuna budi kulisoma na kulitumia katika kila hali tunayokabiliana nalo, Neno la Mungu lina ahadi na ujumbe kwa kila hali unayokutana nayo duniani na kwa kila changamoto na vikwazo, tafuta ahadi za Mungu na kujifunza kuwa ni jinsi gani Mungu anaweza kutusaidia kupitia hali inayotunzunguka ndani ya neno kumejaa mifano ya jinsi Mungu alivyowasaidia wengine na wakaweza kupenya atakusaidia na wewe katika kila hali inayokukabili!



4.       Kumbuka Roho Mtakatifu.

Bwana Yesu alipokuwa akiwaaga wanafunzi wake na kuwajulisha kuwa watapitia vikwazo vingi, wengi wao walijawa na huzini na kiwewe, Yesu alikuwa anafahamu kuwa watapitia changamoto mbalimbali na kuwa wanahitaji msaada wake aliwaahidi kuwa Roho Mtakatifu atakuwa msaada ulio karibu na hivyo mara kwa mara aliwakumbusha kuwa atawaombea ili Baba aweze kuruhusu ujio wa Roho Mtakatifu ambaya atakuwa msaada ulio karibu kama Yesu mwenyewe ona :- Yohana 14:16-17, Nami nitamwomba Baba, naye atawapa Msaidizi mwingine, ili akae nanyi hata milele; ndiye Roho wa kweli; ambaye ulimwengu hauwezi kumpokea, kwa kuwa haumwoni wala haumtambui; bali ninyi mnamtambua, maana anakaa kwenu, naye atakuwa ndani yenu.”  Ni kwa msingi huu nyakati za kanisa la kwanza waliweza kuwa washindi katika majaribu na shida za namna mbalimbali kwa sababu Roho Mtakatifu aliwatia nguvu kukabuiliana na changamoto hizo ona Matendo 4:1-10 “Hata walipokuwa wakisema na watu wale, makuhani na akida wa hekalu na Masadukayo wakawatokea, wakifadhaika sana kwa sababu wanawafundisha watu na kuhubiri katika Yesu ufufuo wa wafu. Wakawakamata, wakawaweka gerezani hata asubuhi; kwa kuwa imekwisha kuwa jioni. Lakini wengi katika hao waliosikia lile neno waliamini; na hesabu ya watu waume ikawa kama elfu tano.Hata asubuhi wakubwa na wazee na waandishi wakakusanyika Yerusalemu,  na Anasi Kuhani Mkuu, na Kayafa pia, na Yohana na Iskanda, na wote wale waliokuwa jamaa zake Kuhani Mkuu.Walipowaweka katikati wakawauliza, Kwa nguvu gani na kwa jina la nani ninyi mmefanya haya? Ndipo Petro, akijaa Roho Mtakatifu, akawaambia, Enyi wakubwa wa watu na wazee wa Israeli, kama tukiulizwa leo habari ya jambo jema alilofanyiwa yule mtu dhaifu, jinsi alivyoponywa, jueni ninyi nyote na watu wote wa Israeli ya kuwa kwa jina la Yesu Kristo wa Nazareti, ambaye ninyi mlimsulibisha, na Mungu akamfufua katika wafu, kwa jina hilo mtu huyu anasimama ali mzima mbele yenu. Petro na Yohana waliweza kushinda vikwazo vilivyokuwa vinawakabili kwa sababu waklijaa Roho Mtakatifu, Roho wa bwana aliwasaidia kuwa na ujasiri na kulishuhudia neno la Mungu hata kwa viongozi wa dini waliokuwa wakaidi na waliokuwa kinyume cha Yesu na ndio maana wakati wote Katika nyakati za kanisa la kwanza Mitume na washirika walipotaka kuchagua viongozi moja ya sifa ilikuwa ni kujaa Roho Mtakatifu, kikwazo cha kulihubiri neno kilipowekwa wao waliomba na Mungu Roho Mtakatifu alikuwa juu yao na akawajaza tena na wakalihubiri neno lake kwa ujasiri ona  Matendo ya Mitume 4:23-31 “Hata walipofunguliwa, wakaenda kwa watu wao, wakawapasha habari ya mambo yote waliyoambiwa na wakuu wa makuhani na wazee. Nao waliposikia, wakampazia Mungu sauti zao kwa moyo mmoja, wakisema, Mola, wewe ndiwe Mungu, ndiwe uliyefanya mbingu na nchi na bahari na vitu vyote vilivyomo; nawe ulinena kwa Roho Mtakatifu kwa kinywa cha babaetu Daudi, mtumishi wako, Mbona mataifa wamefanya ghasia, Na makabila wametafakari ubatili?  Wafalme wa dunia wamejipanga, Na wakuu wamefanya shauri pamoja Juu ya Bwana na juu ya Kristo wake. Maana ni kweli, Herode na Pontio Pilato pamoja na Mataifa na watu wa Israeli, walikusanyika katika mji huu juu ya Mtumishi wako mtakatifu Yesu, uliyemtia mafuta,ili wafanye yote ambayo mkono wako na mashauri yako yamekusudia tangu zamani yatokee. Basi sasa, Bwana, yaangalie matisho yao; ukawajalie watumwa wako kunena neno lako kwa ujasiri wote, ukinyosha mkono wako kuponya; ishara na maajabu vifanyike kwa jina la Mtumishi wako mtakatifu Yesu. Hata walipokwisha kumwomba Mungu, mahali pale walipokusanyika pakatikiswa, wote wakajaa Roho Mtakatifu, wakanena neno la Mungu kwa ujasiri.Kumbe basi tunamuhitaji sana Roho Mtakatifu Msaada ulio karibu kutusaidia wakati wa majaribu, vikwazo mtaabu na mateso pamoja na changamoto mbalimbali tunazokutana nazo katika maisha ulimwengu hautatuweza na magumu yake yote tukimtegemea Roho Mtakatifu na kumjaa yeye katika maisha yetu, kumbuka kuwa dhana hii ya msaada kutoka kwa Roho wa Bwana si ya kiagano jipya tu lakini katika agano la kale tunaona hususani katika kitabu cha waamuzi, pale Israel walipopata vipingamizi na kutumikiswa katika nchi ya kanaani na makabila yenye nguvu Mungu aliwainua waamuzi watu ambao aliwajaza Roho wake mtakatify na watu hao wakawa suluhu ya matatizo ya watu wao Munda hauwezi kutosha kumpitia kila mmoja wetu lakini angalia kwa mfanio maisha ya Samson moja ya waamuzi wakubwa sana na wa kipekee waliofaidika na uwepo wa Roho Mtakatifu nyakati za agano la kale ona  Waamuzi 13:24-25 “Basi yule mwanamke akamzaa mtoto mwanamume akamwita jina lake Samsoni, mtoto huyu akakua, Bwana akambarikia. Roho ya Bwana ikaanza kumtaharakisha katika Mahane-dani, katikati ya Sora na Eshtaoli.kumbe Roho Mtakatifu ndani ya maisha ya mwamini ni msaada mkubwa sana wakati wa vikwazo na vipingamizi vya namna mbalimbali, kama unataka kufurahia maisha ya ushindi katika ulimwengu tulio nao tumuombe sana Mungu na kuishi maisha matakatifu ili tuwe na uhusiano ulio karibu na Mungu wetu Roho Mtakatifu, mara kadhaa tumeona katika maisha ya waamuzi na hasa Samsoni kwamba kila alipokutana na vikwzo Roho wa Mungu alikuja kwa nguvu juu yake na kumsaidia kushinda kikwazo Fulani mbele yake ona kwa mfano katika


Waamuzi 14:1-5 “Samsoni akatelemkia Timna, akaona mwanamke huko Timna, mmojawapo wa binti za Wafilisti. Kisha akapanda, akawaambia baba yake na mama yake, akasema, Nimemwona mwanamke huko Timna, mmojawapo wa binti za Wafilisti; basi mnipatie, nimwoe.Ndipo baba yake na mama yake wakamwambia, Je! Hapana mwanamke hata mmoja katika ndugu zako, au katika jamaa zangu zote, hata uende kumwoa mwanamke kwa hawa Wafilisti wasiotahiriwa? Samsoni akamwambia baba yake; Mnipatie huyo, kwa maana ananipendeza sana. Lakini baba yake na mama yake hawakujua ya kuwa jambo hili ni la Bwana; maana alitaka kisa juu ya Wafilisti. Basi wakati ule Wafilisti walikuwa wakiwatawala Israeli. Ndipo Samsoni na baba yake na mama yake wakatelemkia Timna, wakafika mashamba ya mizabibu huko Timna; na tazama, mwana-simba akamngurumia. Roho ya Bwana ikamjilia kwa nguvu, naye akampasua kana kwamba anampasua mwana-mbuzi, wala hakuwa na kitu cho chote mkononi mwake; lakini hakuwaambia baba yake na mama yake aliyoyafanya.“   


Samsoni alipenda Mwanamke wa kifilisti na akazungumza na wazazi wake lakini walijaribu kumpinga mwisho wakakubaliana naye, Biblia inaonyesha kulikuwa na kusudi la Mungu nyuma yake hivyo Samsoni alimtaka mwanamke huyo na walikwenda yeye na baba yake na mama yake lakini njiani mwana simba akamuungurumia Samsoni, simba alisimama kama kikwako kwa Samsoni lakini kwa uweza wa Roho wa Bwana Samsoni alimpasua kama aposuavyo mwana Mbuzi, Roho wa Bwana atatutia nguvu na kutusaidia kila tunapokutana na vikwazo dhidi yetu.


Waamuzi 15:14-16 “Alipofika Lehi, Wafilisti wakapiga kelele walipokutana naye; ndipo roho ya Bwana ikamjia kwa nguvu, na zile kamba zilizokuwa juu ya mikono yake zikawa kama kitani iliyoteketezwa kwa moto, na vile vifungo vyake vikaanguka mikononi mwake. Naye akaona mfupa mbichi wa taya ya punda, akautwaa, akapiga watu elfu kwa mfupa huo; Samsoni akasema, Kwa taya ya punda chungu juu ya chungu, Kwa taya ya punda nimepiga watu elfuunataka maisha ya ushindi fanya ushirika wa kudumu na Roho Mtakatifu jaa Roho Mtakatifu!,


5.       Kumbuka Neema


Ni muhimu kufahamu kuwa ujumbe wa biblia nzima hususani agano jipya la bwana wetu Yesu Kristo unahusiana na neema, ujumbe wa injili ni neema Mungu anaonyesha neema yake kwa kumleta Yesu Kristo katika maisha yetu, ameteseka msalabani kw niaba yetu kwa sababu sisi tusingeliweza, Mungu ametusaidia ametusaidia madhaifu yetu, Neema ni zawadi kubwa kutoka kwa Mungu kwa sababu hiyo basi hakuna tunaloweza kulifanikisha sisi wenyewe bila neema ya Mungu, 2Wakoritho 12:9 “Naye akaniambia, Neema yangu yakutosha; maana uweza wangu hutimilika katika udhaifu. Basi nitajisifia udhaifu wangu kwa furaha nyingi, ili uweza wa Kristo ukae juu yangu.” Unaona neema ni nini neema ni msaada wa upendo na rehema unaotolewa na Mungu kwa wanadamu bila wao kuwa na jambo lolote la kumshawishi, ni uependeleo pasipo kustahili ni kuhesabika kuwa unastahili kupitia kazi ya Yesu Kristo msalabani, Neema ndio iinayotupa kibali hata cha kusogelea uwepo wa Mungu wakati wa maombi ona Waebrania 4:16 “Basi na tukikaribie kiti cha neema kwa ujasiri, ili tupewe rehema, na kupata neema ya kutusaidia wakati wa mahitaji.” Tunapokabiliana na changamoto zozote za maisha namna pekee ya kushinda changamoto hizo ni kuitumainia neema ya Mungu, kumbuka kuwa kuja kwa Yesu duniani ni pamoja na kutuletea neema ona Yohana 1:17  “Kwa kuwa torati ilitolewa kwa mkono wa Musa; neema na kweli zilikuja kwa mkono wa Yesu Kristo.”  Tunaweza kuwa na maisha ya ajabu na upekee mkubwa sana duniani kama tutajaa neema Luka 1:26-30 “Mwezi wa sita, malaika Gabrieli alitumwa na Mungu kwenda mpaka mji wa Galilaya, jina lake Nazareti, kwa mwanamwali bikira aliyekuwa ameposwa na mtu, jina lake Yusufu, wa mbari ya Daudi; na jina lake bikira huyo ni Mariamu.  Akaingia nyumbani kwake akasema, Salamu, uliyepewa neema, Bwana yu pamoja nawe. Naye akafadhaika sana kwa ajili ya maneno yake, akawaza moyoni, Salamu hii ni ya namna gani? Malaika akamwambia, Usiogope, Mariamu, kwa maana umepata neema kwa Mungu. Neema ya Mungu itaweka hofu zote mbali na wewe, neema ya Mungu itakupa fadhili ambazo kila mmoja anazitamani, ukiwa umejaa neema ahupaswi kuogopa, watu waliofahamu umuhimu wa neema mara kadhaa walimuomba Mungu wakimsifu na kujumuisha katika maombi yao kwamba Mungu wetu pamioja na mambo mengie amejaa neema Zaburi 103:8-10 “Bwana amejaa huruma na neema, Haoni hasira upesi, ni mwingi wa fadhili. Yeye hatateta sikuzote, Wala hatashika hasira yake milele. Hakututenda sawasawa na hatia zetu, Wala hakutulipa kwa kadiri ya maovu yetu.” Kwa msingi huo wakati tunapopitia majaribu na changamoto za aina mbalimbali na jambo lolote lile ambalo kwalo twaliona kuwa ni kikwazo katika maisha yetu ni vema tukakumbuka neema ya Mungu, tukikaribie kiti chake cha rehema kwa ujarisi ili atupatie neema ya kutusaidia wakati wa mahitaji. Yesu alifanikiwa sana katika siku zako zote za maisha yake Duniani kwa sababu alikuwa amejaa neema ona Luka 2:40 “Yule mtoto akakua, akaongezeka nguvu, amejaa hekima, na neema ya Mungu ilikuwa juu yake.” Unaona ili maisha yetu yaweze kuwa na mafanikio ya kila namna tunahitaji neema neno neema katika kiibrania ni CHEN yaani maana yake fadhili, wema kupendelewa na kupewa thamani kubwa na Mungu, na kwa kiyunani neno neema ni CHARIS yaani Msukumo wa Mungu ndani yako unaona, kutokana na hali hii watu walioelewa umuhimu wa neema katika nyakati za agano jipya neema ilikuwa ni moja ya salamu yenye kutakiana Baraka za Mungu hebu jiombee neema kila unapokutana na changamoto na neema hiyo itakubeba!


6.       Kumbuka Imani               

Mara kwa mara Yesu aliwakemea sana wanafunzi wake kwa kutokuwa na imani, aliwaona kuwa hawataweza kukabuiliana na changamoto mbalimbali kama watakosa imani na kwa msingi huo linapokuja swala la kumuamini Mungu Yesu aliwataka wanafunzi wake wawe na imani Mungu hana furaha na mtu anayesita sita ona Waebrania 10:38-39 “Lakini mwenye haki wangu ataishi kwa imani; Naye akisita-sita, roho yangu haina furaha naye. Lakini sisi hatumo miongoni mwao wasitao na kupotea, bali tumo miongoni mwa hao walio na imani ya kutuokoa roho zetu.” Watu wote walioshinda changamoto za aina mbalimbali duniani walikuwa watu wa imani ona Waebrania 11:32-38 “Nami niseme nini tena? Maana wakati usingenitosha kuleta habari za Gideoni na Baraka na Samsoni na Yeftha na Daudi na Samweli na za manabii; ambao kwa imani walishinda milki za wafalme, walitenda haki, walipata ahadi, walifunga vinywa vya simba, walizima nguvu za moto, waliokoka na makali ya upanga. Walitiwa nguvu baada ya kuwa dhaifu, walikuwa hodari katika vita, walikimbiza majeshi ya wageni. Wanawake walipokea wafu wao waliofufuliwa. Lakini wengine waliumizwa vibaya hata kuuawa, wasikubali ukombozi, ili wapate ufufuo ulio bora; wengine walijaribiwa kwa dhihaka na mapigo, naam, kwa mafungo, na kwa kutiwa gerezani; walipigwa kwa mawe, walikatwa kwa misumeno, walijaribiwa, waliuawa kwa upanga; walizunguka-zunguka wakivaa ngozi za kondoo na ngozi za mbuzi; walikuwa wahitaji, wakiteswa, wakitendwa mabaya; (watu ambao ulimwengu haukustahili kuwa nao), walikuwa wakizunguka-zunguka katika nyika na katika milima na katika mapango na katika mashimo ya nchi.”  Imani ni silaha, imani ina nguvu kubwa sana na inatuwezesha kufanya mambo mengi na makubwa sana katika ulimwengu wa roho ona Mathayo 21:21-22 “Yesu akajibu, akawaambia, Amin, nawaambia Mkiwa na imani, msipokuwa na shaka, mtafanya si hilo la mtini tu, lakini hata mkiuambia mlima huu, Ng'oka, ukatupwe baharini, litatendeka. Na yo yote mtakayoyaomba katika sala mkiamini, mtapokea.” Kwa msingi huo kila mwanafunzi wa Biblia anapaswa kuwa mtu wa imani, tukikosa imani kwa Mungu tutajikuta tunashindwa na kusababisha aibu kubwa katika maisha yetu, kamwe tusikubali kuwa watu wasio na imani amini Mungu ya kuwa atakufikisha katika jambo alilolikusudia katika maisha yako, kutokuamini ni machukizo mbele za Mungu na kunaweza kusababisha ukajikuta unaangamizwa au unakataliwa, Imani katika Mungu na ushindi itatupatia thawabu kubwa sana na tutafanikiwa!



7.       Kumbuka maombi.

Wafilipi 4:6-7 “Msijisumbue kwa neno lo lote; bali katika kila neno kwa kusali na kuomba, pamoja na kushukuru, haja zenu na zijulikane na Mungu. Na amani ya Mungu, ipitayo akili zote, itawahifadhi mioyo yenu na nia zenu katika Kristo Yesu.” Wote tunafahamu kuwa Neno la Mungu limetufunza kivitendo kwamba maombi yana nguvu na uwezo mkubwa sana wa kubadilisha mambo, kila wakati Yesu na hata mitume walitutaka tukumbuke kuomba Petro alisema na tumtwike yeye fadhaa zetu zote maana anajishughulisha sana na mambo yetu  angalia katika 1Petro 5:6-7. “Basi nyenyekeeni chini ya mkono wa Mungu ulio hodari, ili awakweze kwa wakati wake; huku mkimtwika yeye fadhaa zenu zote, kwa maana yeye hujishughulisha sana kwa mambo yenu.Unaona hii maana yake ni kuwa hatupaswi kusumbuka wala kufadhaika kazi yetu ni moja kila tunapokutana na changamoto za aina mbalimbali tukumbuke kuomba na tuingie kwenye maombi na kuliitia jina la Mungu wetu naye atatusikia tusijali kuwa nini kinanenwa juu yetu au tunatishiwa kwa kiwango gani sisi tukumbuke kuwa kuna majibu katika maombi, Nabii Daniel alikuwa moja wapo ya watu waliokutana na changamoto za aina mbalimbali katika maisha yake lakini alifahamu wazi kuwa dawa ya kuzishinda changamoto hizo ilikuwa ni kumuomba Mungu aliye hai ona katika  Daniel 6:10-11Hata Danieli, alipojua ya kuwa yale maandiko yamekwisha kutiwa sahihi, akaingia nyumbani mwake, (na madirisha katika chumba chake yalikuwa yamefunguliwa kukabili Yerusalemu;) akapiga magoti mara tatu kila siku, akasali, akashukuru mbele za Mungu wake, kama alivyokuwa akifanya tokea hapo. Basi watu hao wakakusanyika pamoja, wakamwona Danieli akiomba dua, na kusihi mbele za Mungu wake.” Tunajifunza pia katika maisha ya mfalme Hezekia alikuwa ni mfalme aliyemcha Mungu na kujaribu kwa kiwango Fulani kufuata njia za Daudi katika utawakla wake alipokutana na changamoto hata za kiafya aliuelekeza uso wake kwa Mungu bila kujali mazingira aliamini kuwa mazingira ya kuomba yatabadili kabisa hali inayomkabili bila kujali kuwa hatari ya kufa imetangazwa na nani ona  2Wafalme 20:1-6 “Siku hizo Hezekia akaugua, akawa katika hatari ya kufa. Isaya, nabii, mwana wa Amozi, akamjia akamwambia, Bwana asema hivi, Tengeza mambo ya nyumba yako; maana utakufa, wala hutapona. Basi Hezekia akajigeuza, akaelekeza uso wake ukutani, akamwomba Bwana akasema, Nakusihi, Bwana, ukumbuke sasa, jinsi nilivyokwenda mbele zako katika kweli na kwa moyo mkamilifu, na kutenda yaliyo mema machoni pako. Hezekia akalia sana sana. Ikawa, kabla Isaya hajatoka katika mji wa kati, neno la Bwana likamjia, kusema, Rudi, ukamwambie Hezekia, mkuu wa watu wangu, Bwana, Mungu wa Daudi baba yako asema hivi, Nimeyasikia maombi yako, na kuyaona machozi yako; tazama, nitakuponya; siku ya tatu utapanda nyumbani kwa Bwana. Tena, nitazizidisha siku zako, kiasi cha miaka kumi na mitano, nami nitakuokoa wewe, na mji huu, na mkono wa mfalme wa Ashuru, nami nitaulinda mji huu kwa ajili yangu, na kwa ajili ya Daudi, mtumishi wangu.” Maombi yana uwezo mkubwa sana katika maisha yetu, kila aina ya dhiki, kikwazo au changamoto yoyote inaweza kusawazishwa kwa kupitia maombi. Ni kuomba ndiko kutakakotupa ufunguo wa tatizo letu lolote tunalolipitia, Hezekia alikuwa na uzoefu kuwa Mungu anaweza kumponya na janga lililokuwa likimkabili, kwa sababu hata alipopata vitisho kutoka kwa mfalme wa Ashuru aliliitia jina la Bwana kwenye maombi na Mungu alimsikia na kuingilia kati ona  2Nyakati 32:9-22 “Na baada ya hayo Senakeribu mfalme wa Ashuru, akatuma watumishi wake waende Yerusalemu, (naye alikuwapo mbele ya Lakishi, na uwezo wake wote pamoja naye,) kwa Hezekia, mfalme wa Yuda, na kwa Yuda wote waliokuwako Yerusalemu, kusema, Senakeribu, mfalme wa Ashuru, asema hivi, Mwatumainia nini hata mkae mkihusuriwa katika Yerusalemu? Siye Hezekia anayewashawishi, mtolewe kufa kwa njaa na kwa kiu, akisema, Bwana, Mungu wetu, atatuokoa na mkono wa mfalme wa Ashuru?  Si yeye Hezekia huyo aliyeondoa mahali pake pa juu, na madhabahu zake, akawaamuru Yuda na Yerusalemu, akisema, Abuduni mbele ya madhabahu moja, na juu yake mtafukiza uvumba? Je! Ninyi hamjui mimi na baba zangu tuliyowafanyia watu wote wa nchi? Je! Miungu ya mataifa wa nchi iliweza kuokoa kwa lo lote nchi zao na mkono wangu? Ni yupi miongoni mwa miungu ya mataifa wale walioharibiwa kabisa na baba zangu, aliyeweza kuwaokoa watu wake na mkono wangu, hata Mungu wenu aweze kuwaokoa ninyi na mkono wangu?  Basi sasa asiwadanganye Hezekia, wala asiwashawishi kwa hayo, wala msimwamini; kwa kuwa hapana mungu wa taifa lo lote, wala wa ufalme wo wote, aliyeweza kuwaokoa watu wake na mkono wangu, au na mkono wa baba zangu; sembuse Mungu wenu atawaokoaje ninyi na mkono wangu? Na watumishi wake wakazidi kusema juu ya Bwana Mungu, na juu ya Hezekia, mtumishi wake.Tena akaandika waraka, kumtukana Bwana, Mungu wa Israeli, na kumwambia, akisema, Kama vile miungu ya mataifa wa nchi isivyowaokoa watu wao na mkono wangu, vivyo hivyo Mungu wa Hezekia hatawaokoa watu wake na mkono wangu. Wakawalilia kwa sauti kuu, kwa lugha ya Kiyahudi, watu wa Yerusalemu waliokuwako ukutani ili kuwaogofisha, na kuwafadhaisha; hata wapate kuutwaa mji. Wakamnenea Mungu wa Yerusalemu, kana kwamba kuitaja miungu ya mataifa wa nchi, iliyo kazi ya mikono ya watu. Na kwa ajili ya hayo Hezekia mfalme, na Isaya nabii, mwana wa Amozi, wakaomba, wakalia hata mbinguni. Naye Bwana akatuma malaika aliyewakatia mbali mashujaa wote, na majemadari, na maakida, matuoni mwa mfalme wa Ashuru. Basi akarudia nchi yake mwenye haya ya uso. Naye alipoingia nyumbani mwa mungu wake, wale waliotoka viunoni mwake mwenyewe wakamwangamiza humo kwa upanga. Ndivyo Bwana alivyomwokoa Hezekia, na wenyeji wa Yerusalemu, na mkono wa Senakeribu, mfalme wa Ashuru, na mikononi mwa wote, akawaongoza pande zote.Muda hungeweza kutosha kuweza kuonyesha nguvu ya maombi lakini shuhuda hizi chache katika maandiko na zitutoshe kuweza kuonyesha kuwa namna pekee ya kushinda vikwazo vya aina yoyote katika ulimwengu tulio nao ni pamoja na maombi, wakati wowowte tunapokutana na changamoto za aina yoyote ile na tuliitie jina la Bwana naye atatuokoa narudia tena changamoto za aina yoyote!



8.       Kumbuka unyenyekevu.

Moja ya njia ya Mungu ya kutuwezesha kushinda vikwazo na kutupatia neema ni kukumbuka unyenyekevu, Kutembea kwa unyenyekevu kuna faida kubwa sana katika maisha ya mwanadamu, Tatizo kubwa linaloonekana kwa watu wengi sana leo ni kujiamini kunakopitiliza kawaida, ni ukweli ulio wazi kuwa kokosa unyenyekevu kunaleta madhara makubwa sana kuliko unyenyekevu wenyewe, utafiti unaonyesha kuwa watu wanyenyekevu pia wana kiwango kikubwa sana cha self control yaani kujidhibiti, Biblia inatuelekeza na kutufundisha faida kadhaa za unyenyekevu.


a.       Unyenyekevu unaifanya neema ya Mungu kuwa kubwa kwetu Mithali 3:34 “Hakika yake huwadharau wenye dharau, Bali huwapa wanyenyekevu neema.” Kinyume cha unyenyekevu ni kiburi na tunapokuwa na kiburi na Mungu anatupinga na kuondoa neema yake kwetu


b.      Mungu huwapinga wenye kiburi ona 1Petro 5:5-6 “Vivyo hivyo ninyi vijana, watiini wazee. Naam, ninyi nyote jifungeni unyenyekevu, mpate kuhudumiana; kwa sababu Mungu huwapinga wenye kiburi, lakini huwapa wanyenyekevu neema. Basi nyenyekeeni chini ya mkono wa Mungu ulio hodari, ili awakweze kwa wakati wake;” 


c.       Kiburi huambatana na fedhea na aibu Mithali 11:2 “Kijapo kiburi ndipo ijapo aibu; Bali hekima hukaa na wanyenyekevu.” 


d.      Unyenyekevu unakufanya uinuliwe juu sana na Mungu Wafilipi 2:6-11 “ambaye yeye mwanzo alikuwa yuna namna ya Mungu, naye hakuona kule kuwa sawa na Mungu kuwa ni kitu cha kushikamana nacho; bali alijifanya kuwa hana utukufu, akatwaa namna ya mtumwa, akawa ana mfano wa wanadamu; tena, alipoonekana ana umbo kama mwanadamu, alijinyenyekeza akawa mtii hata mauti, naam, mauti ya msalaba. Kwa hiyo tena Mungu alimwadhimisha mno, akamkirimia Jina lile lipitalo kila jina; ili kwa jina la Yesu kila goti lipigwe, la vitu vya mbinguni, na vya duniani, na vya chini ya nchi; na kila ulimi ukiri ya kuwa YESU KRISTO NI BWANA, kwa utukufu wa Mungu Baba. Unyenyekevu sio ujinga ni hekima Mungu atatuinua wakati wa vikwazo kama tutakumbuka kutembea kwa unyenyekvu mbele zake na kujilinda na kiburi.



9.       Kumbuka uvumilivu.



Changamoto nyingine tunazokutana nazo duniani zinahitaji uvumilivu na subira, wakati mwingine itatuchukua muda mrefu kusubiria kutimizwa kwa ahadi za Mungu wetu katika maisha yetu kwa msingi huo tutajitaji uvumilivu, wengi wetu tunapenda kuona mambo yanatokea kwa haraka katika maisha yetu lakini Mungu anazo njia zake na mojawapo ni kututaka tutembee katika uvumilivu yako mabo mengine hayatokei kwa haraka mpaka tuwe na subira  neno uvumilivu katika kiingereza linatumika neno Persevearence  ambalo maana yake kwa kiingereza ni doing something despite of difficulty or delay in achieving success tunaweza kusema kwa Kiswahili ni hali ya kuendelea kuwa na subira bila kujali muda wala ugumu wa jambo katika kufikia mafanikio Waebrania 12:1-3 “Basi na sisi pia, kwa kuwa tunazungukwa na wingu kubwa la mashahidi namna hii, na tuweke kando kila mzigo mzito, na dhambi ile ituzingayo kwa upesi; na tupige mbio kwa saburi katika yale mashindano yaliyowekwa mbele yetu, tukimtazama Yesu, mwenye kuanzisha na mwenye kutimiza imani yetu; ambaye kwa ajili ya furaha iliyowekwa mbele yake aliustahimili msalaba na kuidharau aibu, naye ameketi mkono wa kuume wa kiti cha enzi cha Mungu.Maana mtafakarini sana yeye aliyeyastahimili mapingamizi makuu namna hii ya watendao dhambi juu ya nafsi zao, msije mkachoka, mkizimia mioyoni mwenu.” Unaweza kuona neno la Mungu linatutaka kustahimili yaani kuvumilia wakati wote tunapopita katika vikwazo, magumu na majaribu ya aina mbalimbali tunapaswa kumuamini Mungu na kuendelea kuwa na subira bila kupoteza matumaini, Mungu anamengi ambayo ametuhifadhia na ana mpango wake kwa kila mtihani tunaoupitia na wakati mwingine kupitia magumu hayo atatokeza mema mbele yetu, Yakobo 5:10-11 “Ndugu, watwaeni manabii walionena kwa jina la Bwana, wawe mfano wa kustahimili mabaya, na wa uvumilivu. Angalieni, twawaita heri wao waliosubiri. Mmesikia habari ya subira yake Ayubu, mmeuona mwisho wa Bwana ya kwamba Bwana ni mwingi wa rehema, mwenye huruma.”      

      

10.   Kumbuka furaha.

Mojawapo ya kikwazo kikubwa sana cha mafanikio yetu ni kukubali kuhuzunika, huzuni inaathiri uwezo wetu wa kufikiri, inatufanya tukate tamaa na kufikiri kuwa mwisho umefika usikubali kutawaliwa na huzuni wakati wa changamoto unazozipitia, maandiko yanatutaka tuwe na furaha wakati tunapopitia changamoto za aina mbalimbali ona Yakobo 1:2-4  “Ndugu zangu, hesabuni ya kuwa ni furaha tupu, mkiangukia katika majaribu mbalimbali; mkifahamu ya kuwa kujaribiwa kwa imani yenu huleta saburi. Saburi na iwe na kazi kamilifu, mpate kuwa wakamilifu na watimilifu bila kupungukiwa na neno.” Endapo una adui usikubali kumuonyesha adui yako machozi, wakati wote mtegemee Mungu na hakikisha kuwa unafuraha siku zote hili ndio agizo la neno la Mungu Wafilipi 4:4 “Furahini katika Bwana sikuzote; tena nasema, Furahini.



11.   Kumbuka Mapenzi ya Mungu.


Maisha hayako chini ya udhibiti wetu, kwa hivyo hatupaswi kijisumbua katika jambo lolote neno la Mungu linasema Mathayo 6:25-27 “Kwa sababu hiyo nawaambieni, Msisumbukie maisha yenu, mle nini au mnywe nini; wala miili yenu, mvae nini. Maisha je! Si zaidi ya chakula, na mwili zaidi ya mavazi? Waangalieni ndege wa angani, ya kwamba hawapandi, wala hawavuni, wala hawakusanyi ghalani; na Baba yenu wa mbinguni huwalisha hao. Ninyi je! Si bora kupita hao? Ni yupi kwenu ambaye akijisumbua aweza kujiongeza kimo chake hata mkono mmoja? Hatuna budi kujiachia katika mapenzi ya Mungu yako mambo ambayo hayako chini ya uwezo wetu yako kwenye mikono ya Mungu hatuwezi kuyadhibiti nsisi wenyewe kwa hiyo ni muhimu kwetu kumuachia Mungu ayashikilie na hayo ndio mapenzi yake, Mapenzi ya Mungu ni ngumu kuyatambua wakati mwingine na hayaelezeki wala huwezi kuuliza kwa nini lakini la msingi ni kuendelea kuamini kuwa Mungu yuko nyuma ya mambo kutusaidia na kutiokeza mema Warumi 8:28-30 “Nasi twajua ya kuwa katika mambo yote Mungu hufanya kazi pamoja na wale wampendao katika kuwapatia mema, yaani, wale walioitwa kwa kusudi lake.  Maana wale aliowajua tangu asili, aliwachagua tangu asili wafananishwe na mfano wa Mwana wake, ili yeye awe mzaliwa wa kwanza miongoni mwa ndugu wengi. Na wale aliowachagua tangu asili, hao akawaita; na wale aliowaita, hao akawahesabia haki; na wale aliowahesabia haki, hao akawatukuza. Mungu anajua makusudi na mapenzi yake kwa nini aruhusu kupitia unachokipitia yeye anajua kwa undani zaidi, na anajua lililosahihi pale atakapokuja kukufunulia mapenzi yake utakuja kuelewa ni kwanini aliruhusu alichokiruhusu katika maisha yako na kwa nini Mungu alikuacha upitie hilo kwa hivyo ni muhimu kwetu kukubali ilikuwa ni njia ya Mungu kupitia unachokipitia Mwanzo 50:15-20 “Ndugu zake Yusufu walipoona ya kwamba baba yao amekufa, walisema, Labda Yusufu atatuchukia; naye atatulipa maovu yetu tuliyomtenda. Wakapeleka watu kwa Yusufu, kunena, Baba yako alitoa amri kabla ya kufa kwake, akasema, Mwambieni Yusufu hivi, Naomba uwaachilie ndugu zako kosa lao na dhambi yao, maana walikutenda mabaya; sasa twakuomba utuachilie kosa la watumwa wa Mungu wa baba yako. Yusufu akalia waliposema naye. Nduguze wakaenda tena, wakamwangukia miguu, wakasema, Tazama, sisi tu watumwa wako.Yusufu akawaambia, Msiogope, je! Mimi ni badala ya Mungu? Nanyi kweli mlinikusudia mabaya, bali Mungu aliyakusudia kuwa mema, ili itokee kuokoa taifa kubwa, kama ilivyo leo.” Angalia mapito yote ya Yusufu na kumbuka mapito aliyoyapitia na angalia mwisho wake ilikuwa njia ya Mungu kumfikisha hapo alipomfikisha kumbe ilikuwa ni njia ya Mungu kumleta katika ngazi hii japo Mungu alitumia njia mbaya ya ndugu zake kumleta hapo alipomleta



12.   Kumbuka kuto-kunungu’nika


Manung’uniko ni moja ya tabia ambayo inafunga Baraka za Mungu, au kuzichelewesha kwetu, Biblia inatutaka tuache kuning’unikiana sisi kwa sisi Yohana 6:43 “Basi Yesu akajibu, akawaambia, Msinung'unike ninyi kwa ninyi.Manunguniko yanaweza kuleta adhabu kutoka kwa Mungu 1Wakoritho 10:10 “Wala msinung'unike, kama wengine wao walivyonung'unika, wakaharibiwa na mharabu.” Mungu anachukizwa sana na Manung’uniko, manung’uniko kwa sababu manung’uniko kwake ni sawa na 

a.       Kukosa imani
b.      Kusahahu matendo ya Mungu
c.       Hayaondoai tatizo bali yanavunja moyo wengine
d.      Yanaleta ushuhuda mbaya
e.      Yanampa shetani  nafasi ya kulaumu 

Kwa kulijua hili neno la Mungu limetuonya tuacha kabisa kunung’unika na badala yake tumtukuze Mungu na kumshukuru kwa kila jambo, Mitume walikazia sana nyakati za kanisa la kwanza watu waache kunung’unika manung’uniko ni dhambi 

Wafilipi 2:13-15 “Kwa maana ndiye Mungu atendaye kazi ndani yenu, kutaka kwenu na kutenda kwenu, kwa kulitimiza kusudi lake jema.Yatendeni mambo yote pasipo manung'uniko wala mashindano, mpate kuwa wana wa Mungu wasio na lawama, wala udanganyifu, wasio na ila kati ya kizazi chenye ukaidi, kilichopotoka; ambao kati ya hao mnaonekana kuwa kama mianga katika ulimwengu,”      
      
Yakobo 5:9 “Ndugu, msinung'unikiane, msije mkahukumiwa. Angalieni, mwamuzi amesimama mbele ya milango.” 

1Petro 4:8-11 “Zaidi ya yote iweni na juhudi nyingi katika kupendana; kwa sababu upendano husitiri wingi wa dhambi. Mkaribishane ninyi kwa ninyi, pasipo kunung'unika; kila mmoja kwa kadiri alivyoipokea karama, itumieni kwa kuhudumiana; kama mawakili wema wa neema mbalimbali za Mungu.  Mtu akisema, na aseme kama mausia ya Mungu; mtu akihudumu, na ahudumu kwa nguvu anazojaliwa na Mungu; ili Mungu atukuzwe katika mambo yote kwa Yesu Kristo. Utukufu na uweza una yeye hata milele na milele. Amina.” Wana wa Israel mara kwa mara walijikosesha Baraka za Mungu kwa sababu ya manung’uniko yao, Manunguniko yanaweza kujibiwa lakini kwa kawaida yanajibiwa vibaya Hesabu 11:1-2 “Kisha hao watu walikuwa kama wanung'unikao, wakinena maovu masikioni mwa Bwana; Bwana aliposikia hayo, hasira zake zikawaka; na moto wa Bwana ukawaka kati yao, ukateketeza katika mipaka ya mwisho wa marago. Ndipo watu wakamlilia Musa; naye Musa akamwomba Bwana, na ule moto ukakoma.”


13.   Kumbuka Jina la Yesu.


1Samuel 17: 45 “Ndipo Daudi akamwambia yule Mfilisti, Wewe unanijia mimi na upanga, na fumo, na mkuki, bali mimi ninakujia wewe kwa jina la Bwana wa majeshi, Mungu wa majeshi ya Israeli uliowatukana.”  Moja ya siri kubwa sana aliyoitumia Daudi kupata ushindi dhidi ya Adui yake na wa taifa lake ni Jina la Bwana Mungu wa majeshi, Jina hili Nyakati za agano la kale lilikuwa limefichwa sana na lilikuwa ni siri kubwa mno, lakini katika nyakati za agano jipya jina hili tumepewa ni jina lanye kifurushi cha wokovu ni jina pekee linaloweza kumuokoa awaye yote atakayeliitia. Matendo 4:10-12jueni ninyi nyote na watu wote wa Israeli ya kuwa kwa jina la Yesu Kristo wa Nazareti, ambaye ninyi mlimsulibisha, na Mungu akamfufua katika wafu, kwa jina hilo mtu huyu anasimama ali mzima mbele yenu. Yeye ndiye jiwe lile lililodharauliwa na ninyi waashi, nalo limewekwa kuwa jiwe kuu la pembeni. Wala hakuna wokovu katika mwingine awaye yote, kwa maana hapana jina jingine chini ya mbingu walilopewa wanadamu litupasalo sisi kuokolewa kwalo.”Jina la Yesu ni jina la kipekee sana na Mungu ametupa jina hili ili tuweze kulitumia kwaajili ya utukufu wake, tunapokutana na magumu na changamoto mbali mbali liko jina la Yesu, ni jina la pakee sana Marko 16:15-18 “Akawaambia, Enendeni ulimwenguni mwote, mkaihubiri Injili kwa kila kiumbe. Aaminiye na kubatizwa ataokoka; asiyeamini, atahukumiwa. Na ishara hizi zitafuatana na hao waaminio; kwa jina langu watatoa pepo; watasema kwa lugha mpya; watashika nyoka; hata wakinywa kitu cha kufisha, hakitawadhuru kabisa; wataweka mikono yao juu ya wagonjwa, nao watapata afya.” Unaweza kuona Yesu mwenyewe amatuamuru kwamba kwa jina lake tunaweza kutatua matatizo na majaribu na changamoto za aina mbalimbali, Jina lake lina nguvu, na lina mamlaka kubwa sana ya kupambana na hali ngumu za namna yoyote, Jina hili ni ngome ambalo tunaweza kulitumainia na tukawa Salama Mithali 18:10 “Jina la Bwana ni ngome imara; Mwenye haki huikimbilia, akawa salama.” Kwa kuhitimisha ni muhimu kufahamu kwamba jina la Yesu ni jina lililoinuliwa sana na lina uwezo mkubwa na kwa sababu hiyo zungumza kwa ujasiri na kwa mamlaka kwani jina hili ni silaha kubwa na hakuna vita utaishindwa ukilitumia jina la Yesu! 


14.   Kumbuka kujitenga/kujiepusha (to withdrw) 


Ni muhimu kufahamu kuwa mojawapo ya njia ya kujihami na vikwazo vya aina mbalimbali ni pamoja na kujitenga au kujitoa au kujiepusha njia kama hii inaweza wakati mwingine kutuletea amani na njia kama hii ilitumiwa pia na wazee wetu Abraham na Lutu ona  Mwanzo 13:2-13Naye Abramu alikuwa ni tajiri sana kwa mifugo, kwa fedha, na kwa dhahabu. Akaendelea kusafiri kutoka kusini mpaka Betheli, mahali pale palipokuwapo hema yake kwanza kati ya Betheli na Ai; napo ndipo palipokuwa na madhabahu aliyofanya hapo kwanza; naye Abramu akaliitia jina la BWANA hapo. Na Lutu aliyesafiri pamoja na Abramu, yeye naye alikuwa na makundi ya ng'ombe na kondoo, na hema. Na ile nchi haikuwatosha, ili wakae pamoja; maana mali zao zilikuwa nyingi, hata wasiweze kukaa pamoja. Kukawako ugomvi kati ya wachunga wanyama wa Abramu, na wachunga wanyama wa Lutu; na siku zile Wakanaani na Waperizi walikuwa wakikaa katika nchi. Abramu akamwambia Lutu, Basi, usiwepo ugomvi, nakusihi, kati ya mimi na wewe, wala kati ya wachungaji wangu na wachungaji wako; maana sisi tu ndugu. Je! Nchi hii yote haiko mbele yako? Basi ujitenge nami, nakusihi; ukienda upande wa kushoto, nitakwenda upande wa kuume; ukienda upande wa kuume, nitakwenda upande wa kushoto. Lutu akainua macho yake, akaliona Bonde lote la Yordani, ya kwamba lote pia lina maji, kabla BWANA hajaharibu Sodoma na Gomora, lilikuwa kama bustani ya BWANA, kama nchi ya Misri hapo unapokwenda Soari. Basi Lutu akajichagulia Bonde lote la Yordani; Lutu akasafiri kwenda upande wa mashariki; wakatengana wao kwa wao. Abramu akakaa katika nchi ya Kanaani, na Lutu akakaa katika miji ya lile Bonde; akajongeza hema yake mpaka Sodoma.Lakini watu wa Sodoma walikuwa wabaya, wenye kufanya dhambi nyingi sana juu ya BWANA. BWANA akamwambia Abramu, alipokwisha kutengana na Lutu, Inua sasa macho yako, ukatazame kutoka hapo ulipo, upande wa kaskazini, na wa kusini na wa mashariki na wa magharibi; maana nchi hii yote uionayo, nitakupa wewe na uzao wako hata milele.” Unaweza kuona sio lazima ung’ang’ane kitu wakati mwingine kujiepusha kunaweza kuleta suluhu ya kudumu na amani ya kudumu miongoni mwa pande zenye migogoro, jiepushe, aidha maandiko yanatufunza namna Isaka naye alivyokuwa mtu mwema na mwenye kujiepusha na migogoro ya mara kwa mara, akiwa na Abimeleki, walfilistio mara kwa mara walidai kisima alichochimba Isaka  ni chao wakagombania lakini yeye alijiepusha na kuchimba kingine Mungu alimstawisha sana Mwanzo 26:16-22 “Abimeleki akamwambia Isaka, Utoke kwetu, maana wewe una nguvu sana kuliko sisi.Basi Isaka akatoka huko akapiga kambi katika bonde la Gerari, akakaa huko.Isaka akarudi akavichimbua vile visima vya maji walivyovichimba siku za Ibrahimu babaye; maana wale Wafilisti walikuwa wamevifukia baada ya kufa kwake Ibrahimu; naye akaviita majina kufuata majina alivyoviita babaye. Watumwa wa Isaka wakachimba katika lile bonde, wakapata kisima cha maji yanayobubujika. Wachungaji wa Gerari wakagombana na wachungaji wa Isaka wakisema, Maji haya ni yetu. Ndipo akakiita jina la kile kisima Eseki, kwa sababu waligombana naye. Wakachimba kisima kingine, wakagombania na hicho tena. Akakiita jina lake Sitna. Akaondoka huko akachimba kisima kingine, wala hicho hawakukigombania. Akakiita jina lake Rehobothi, akasema, Kwa kuwa sasa BWANA ametufanyia nafasi, nasi tutazidi katika nchi. Tunaweza kuona kuwa wakati mwingine kujitoa kunaweza kuwa sababu ya kuepuka migogoro na kujiondoa katika changamoto kadhaaa kwa makusudi mema tu, Hili ni jambo la kawaida wanapoishi watu na wakati mwingine ikatokea tofauti tunaweza kuamua kujitioa kwa faida ya pande zote mbili na kwa kusudi la kumpa Mungu utukufu, Jambo hili halikuwahi kutokea kwa wazee wetu tu bali hata wakati wa mitume tena wenye sifa kubwa ona Matendo 15:36-40 “Baada ya siku kadha wa kadha Paulo akamwambia Barnaba, Haya! Mrejee sasa tukawaangalie hao ndugu katika kila mji tulipolihubiri neno la Bwana, wa hali gani.Barnaba akaazimu kumchukua Yohana aliyeitwa Marko pamoja nao.Bali Paulo hakuona vema kumchukua huyo aliyewaacha huko Pamfilia, asiende nao kazini. Basi palitokea mashindano baina yao hata wakatengana. Barnaba akamchukua Marko akatweka kwenda Kipro. Lakini Paulo akamchagua Sila, akaondoka, akiombewa na wale ndugu apewe neema ya Bwana.Unaona wakati mwingine hakuna sababu ya kulazimisha mambo, Shamba la Mungu ni pan asana ni kubwa mmno tunaweza kuamua tu ukielekea kaskazini nitaenda kusini, ili amani iwepo na Mungu akapate kutukuzwa, hakuna sababu ya kumzunguka mtu wala kumtesa “make them happy by your absent if your presence makes them not happy” kama uwepo wako ni tatizo kwako wafanya wenye furaha kwa kuondoka kati yao, aidha pia yako maeneo mengine ambayo kwayo Biblia inatuonya kujitoa ili tusiweze kuharibu uhusiano wetu na Mungu Zaburi 1:1 “Heri mtu yule asiyekwenda Katika shauri la wasio haki; Wala hakusimama katika njia ya wakosaji; Wala hakuketi barazani pa wenye mizaha.” Wakati mwingine ili kujihadhari na vikwazo na majaribu na mapito mbalimbali njia sahihi inaweza kuwa kujitenga au kujihadhari au kuondoka Biblia inatutaka tujihadhari na watu wasioendenda kwa utaratibu 2Wathesalonike 3:6-7 “Ndugu, twawaagiza katika jina la Bwana Yesu Kristo, jitengeni nafsi zenu na kila ndugu aendaye bila utaratibu, wala si kwa kufuata mapokeo mliyoyapokea kwetu. Mwajua wenyewe jinsi iwapasavyo kutufuata; kwa sababu hatukuenda bila utaratibu kwenu;Biblia pia imeagiza kujitenga na watu wanaoleta mafarakano na wenye kukwaza watu Warumi 16:17 “Ndugu zangu, nawasihi, waangalieni wale wafanyao fitina na mambo ya kukwaza kinyume cha mafundisho mliyojifunza; mkajiepushe nao.Pia maandiko yanatutaka tujihadhari na kujiepusha na watu wasiotaka kufanya suluhu wasiotaka mapatano 2Timotheo 3:2-5 “Lakini ufahamu neno hili, ya kuwa siku za mwisho kutakuwako nyakati za hatari. Maana watu watakuwa wenye kujipenda wenyewe, wenye kupenda fedha, wenye kujisifu, wenye kiburi, wenye kutukana, wasiotii wazazi wao, wasio na shukrani, wasio safi,wasiowapenda wa kwao, wasiotaka kufanya suluhu, wasingiziaji, wasiojizuia, wakali, wasiopenda mema, wasaliti, wakaidi, wenye kujivuna, wapendao anasa kuliko kumpenda Mungu; wenye mfano wa utauwa, lakini wakikana nguvu zake; hao nao ujiepushe nao.Pia Biblia inatutaka tujiepushe na jambo lolote lile ambalo haklina faida Tito 3:9 “Lakini maswali ya upuzi ujiepushe nayo, na nasaba, na magomvi, na mashindano ya sheria. Kwa kuwa hayana faida, tena hayana maana.” Kumbe basi kujiepusha ni mojawapo ya njia muhimu sana inayoweza kutusaidia kushinda vikwazo vya aina mbalimbali duniani, sio kila kitu kuwa ni lazima ukabiliane nacho vingine vinataka ujiepushe tu!         
                             

15.   Kumbuka kuridhika (To be Content)


Changamoto kubwa sana inayosumbua watu duniani ni kutokuridhika watu wengi wanasumbuliwa na tamaa kwa sababu wanataka kuwa zaidi ya kile walichojaaliwa na Mungu, sio vibaya kunai mambo makubwa lakini ni hatari sana kunai makuu kuliko ikupasavyo kunia, kuwania kuwa nafasi ya kwanza sio jambo baya, kuwania kupata division one sio jambo baya lakini kushindana na Mtu, katika maswala ya mali, fedha na cheo ni tamaa mbaya Warumi 12:1-8 “Basi, ndugu zangu, nawasihi, kwa huruma zake Mungu, itoeni miili yenu iwe dhabihu iliyo hai, takatifu, ya kumpendeza Mungu, ndiyo ibada yenu yenye maana. Wala msiifuatishe namna ya dunia hii; bali mgeuzwe kwa kufanywa upya nia zenu, mpate kujua hakika mapenzi ya Mungu yaliyo mema, ya kumpendeza, na ukamilifu. Kwa maana kwa neema niliyopewa namwambia kila mtu aliyeko kwenu asinie makuu kupita ilivyompasa kunia; bali awe na nia ya kiasi, kama Mungu alivyomgawia kila mtu kiasi cha imani.”  Watu wengi sana nyakati za kanisa la kwanza walitaka kuwa kama Paulo Mtume, lakini yeye aliwaonya kuwa neema aliyopewa yeye ni tofauti, Mungu humpa kila mmoja karama kwa kadiri ya neema tama ya kuwa kama Fulani au kutaka kumzidi Fulani inaweza kutuletea mambo magumu mno kwa hivyo ni muhimu kuridhikana kile ulichonacho Mungu ameahidi kutokutuacha wala kutupungukia kwa hivyo na tumuombe yeye tuishi maisha ya kiasi Waebrania 13:5-6 “Msiwe na tabia ya kupenda fedha; mwe radhi na vitu mlivyo navyo; kwa kuwa yeye mwenyewe amesema, Sitakupungukia kabisa, wala sitakuacha kabisa. Hata twathubutu kusema, Bwana ndiye anisaidiaye, sitaogopa; Mwanadamu atanitenda nini? Kama tutaishi maisha yanayompendeza Mungu na tukaishai maisha ya kuridhika Biblia inasema kuna faida kubwa sana kuliko watu wanaotamkani kuwa na mali kwani wengi huangukia katika mitego ya aina mbalimbali 1Timotheo 6:6-11 “Walakini utauwa pamoja na kuridhika ni faida kubwa. Kwa maana hatukuja na kitu duniani, tena hatuwezi kutoka na kitu;ila tukiwa na chakula na nguo tutaridhika na vitu hivyo. Lakini hao watakao kuwa na mali huanguka katika majaribu na tanzi, na tamaa nyingi zisizo na maana, zenye kudhuru, ziwatosazo wanadamu katika upotevu na uharibifu. Maana shina moja la mabaya ya kila namna ni kupenda fedha; ambayo wengine hali wakiitamani hiyo wamefarakana na Imani, na kujichoma kwa maumivu mengi. Bali wewe, mtu wa Mungu, uyakimbie mambo hayo; ukafuate haki, utauwa, imani, upendo, saburi, upole”. 


Ni muhimu kumsihi Mungu atufundishe kuwa na kiasi, Paulo mtume alifundishwa kuwa radhi katika hali zote hivyo hakukuwa na aina ya maisha yaliyombabaisha wako watu wengine hufa kwa sababu ya mali zao mioyo yao iko katika hizo, lakini kama maandiko yasemavyo hatukuja na kitu duniani wala hatutaondoka na kitu, tukiwanacho kisitupe kiburi wala mabadiliko wala kuinua mabega na tusipokuwa nacho tusimkufuru Mungu ona  Wafilipi 4:11-13 “Si kwamba nasema haya kwa kuwa nina mahitaji; maana nimejifunza kuwa radhi na hali yo yote niliyo nayo. Najua kudhiliwa, tena najua kufanikiwa; katika hali yo yote, na katika mambo yo yote, nimefundishwa kushiba na kuona njaa, kuwa na vingi na kupungukiwa. Nayaweza mambo yote katika yeye anitiaye nguvu.”   

       
                                                                                     
Na Rev. Innocent Kamote
Mkuu wa wajenzi mwenye Hekima
0718990796

ikamote@yahoo.com

Jumanne, 16 Juni 2020

Hata nikamtwaa kuwa mke wangu?


Mwanzo 12:18-19 “Ndipo Farao akamwita Abramu, akasema, N'nini hili ulilonitendea? Mbona hukuniambia ya kuwa huyo ni mkeo? Mbona ulisema, Huyo ni umbu langu, hata nikamtwaa kuwa mke wangu? Basi sasa, huyo mke wako umchukue, uende zako





Utangulizi:


Mojawapo ya Habari za kibiblia ambazo zinazua maswali mengi kwa wanafunzi wa Biblia ni Pamoja na habari ya Abrahamu na Sara Kushuka Misri, kwaajili ya kujihami na njaa iliyotokea katika inchi ya kanaani, wote tunakubaliana kuwa tunaifahamu habari hii, lakini kama wanafunzi wa Biblia tunapoisoma habari hii kuna maswali kadhaa wa kadhaa yanayoibuka kutokana na kisa hiki, mengine yakiwa na majibu na mengine yakituacha katika hali ya utata, Ndio kuna maswali mengi tunaweza kujiuliza mfano, Sara aliyekuwa na miaka 65 wakati huu na bado anaonekana alikuwa mzuri sana kiasi cha kuhatarisha maisha ya Abrahamu?, hii inaweza kukustaajabisha, lakini sio hivyo tu  Abrahamu aliyekuwa baba wa Imani na mtu wa haki anawezaje kusema Uongo? Je alidanganya au alisema ukweli? Aliposema Sara ni dada yangu huku akiwa ni mke wake?, lakini sio hivyo tu anawezaje kumuachia mkewe kirahisi achukuliwe na mtu mwingine?, sio hivyo tu kwa nini swala hili lilijirudia kama mara tatu katika kitabu cha Mwanzo, na nini tunajifunza kutokana na habari ya Sara na Abrahamu kushuka Misri? Lakini swali kubwa na makini zaidi Je Farao alifanikiwa kumfanya Sara kama mke wake? Hili ndio swali zito zaidi kuliko mengine tunapotafakari kitu cha kujifunza!. Kwanza tupate habari kamili:-

Mwanzo 12:10-20 “Basi kulikuwa njaa katika nchi ile; Abramu akashuka Misri, akae huko kwa muda maana njaa ilikuwa nzito katika nchi. Ikawa alipokuwa karibu kuingia Misri, akamwambia Sarai mkewe, Tazama, najua ya kuwa u mwanamke mzuri wa uso; basi itakuwa, Wamisri watakapokuona watasema, Huyu ni mkewe; kisha wataniua mimi na wewe watakuacha hai. Tafadhali useme, wewe u ndugu yangu, iwe heri kwangu kwa ajili yako, na nafsi yangu iishi kwa ajili yako. Basi ikawa Abramu alipofika Misri, Wamisri wakamwona huyo mwanamke ya kwamba yeye ni mzuri sana. Wakuu wa Farao wakamwona, nao wakamsifu kwa Farao; basi yule mwanamke akachukuliwa nyumbani mwa Farao. Naye akamtendea Abramu mema kwa ajili yake; naye alikuwa na kondoo na ng'ombe, na punda waume, na watumwa, na wajakazi, na punda wake, na ngamia.  Lakini BWANA akampiga Farao na nyumba yake mapigo makuu, kwa ajili ya Sarai, mkewe Abramu. Ndipo Farao akamwita Abramu, akasema, N'nini hili ulilonitendea? Mbona hukuniambia ya kuwa huyo ni mkeo? Mbona ulisema, Huyo ni umbu langu, hata nikamtwaa kuwa mke wangu? Basi sasa, huyo mke wako umchukue, uende zako. Farao akawaagiza watu kwa ajili yake, wakampeleka njiani, na mkewe, na kila alichokuwa nacho.”


Kushuka Misri kwa sababu ya Njaa.


Biblia iko wazi kuwa wakati huu sio kuwa Abrahamu alikuwa ameacha kumuamini Mungu hapana, Yeye alikuwa ameshuka Misri kwa sababu ya njaa kali iliyotokea katika nchi ya Kanaani Mwanzo 12:10 “Basi kulikuwa njaa katika nchi ile; Abramu akashuka Misri, akae huko kwa muda maana njaa ilikuwa nzito katika nchi.Ukame wa muda mrefu ulikuwa umeendelea katika mashariki ya kati nyakati za Abrahamu na kuathiri maeneo yote yanayotegema mvua, athari ziliwapata wakulima pamoja na wafugaji pia kwahiyo kwaajili ya mifugo na mahitaji ya chakula Abrahamu aliona vema kwenda Misri na maandiko yako wazi kuwa alikuwa akae kwa muda kwa sababu ya njaa, Lakini pia wote tunakubaliana kuwa Misri tangu miaka mingi walikuwa wanatumia kilimo cha umwagiliaji kutokana na kuwepo kwa bonde la Mto Nile hali kadhalika inawezekana jamii za wafugaji waliteremka pembezoni mwa mto huo kwaajili ya malisho ya wanyama na maji.
Tunajifunza kwamba tunapomtii Mungu haimaanishi kuwa hatutakutana na changamoto za kimaisha ni wazi kuwa Abrahamu alimtii Mungu na kufika katika inchi ile ambayo Mungu alimuonyesha, Abrahamu alikuwa na mke tasa,

Mwanzo 11:30 “Na Sarai alikuwa tasa, hakuwa na mtoto.”,
Lakini pia alikuwa amekwenda mbali sana na familia yake Mwanzo 12:1 “BWANA akamwambia Abramu, Toka wewe katika nchi yako, na jamaa zako, na nyumba ya baba yako, uende mpaka nchi nitakayokuonyesha;” na sasa akiwa amemtii Mungu anakutana na janga la Njaa katika inchi ya kanaani, hatupaswi kuona kuwa ni jambo geni kukutana na changamoto za aina mbalimbali tuwapo duniani pamoja na kuwa tunamtii Mungu, tunaweza kukutana na upinzani mkubwa, mambo magumu na matatizo, Lazima tukubali kuwa tuko duniani na kuwa nayo ni njia ya Mungu ya kutufundisha maswala muhimu, lazima tusonge mbele katika kumtii  na kutimiza kusudi lake 1Petro 4:12-13 “Wapenzi, msione kuwa ni ajabu ule msiba ulio kati yenu, unaowapata kama moto ili kuwajaribu, kana kwamba ni kitu kigeni kiwapatacho.” Unaweza kuwa umefuata taratibu zote katika kuoa kwako lakini ukashangaa ndoa yako ina changamoto lukuki kuliko ya wale walipita shotikati, Mungu anaweza kuwa amesema nawe ufungue huduma kwa sauti ya wazi na ukatii lakini ukakutana na changamoto za ajabu sana kana kwamba si yeye aliyekuita mahali hapo na maswala mengine kadha wa kadha, hayo yasituvunje moyo wala kututoa katika kulitimiza hivyo kusudi la Mungu.

Tafadhali useme, wewe u ndugu yangu


Kama majaribu hayo hayatoshi akiwa Misri sasa Abrahamu anakutana na changamoto nyingine angalia Mwanzo 12:11-16 “Ikawa alipokuwa karibu kuingia Misri, akamwambia Sarai mkewe, Tazama, najua ya kuwa u mwanamke mzuri wa uso; basi itakuwa, Wamisri watakapokuona watasema, Huyu ni mkewe; kisha wataniua mimi na wewe watakuacha hai. Tafadhali useme, wewe u ndugu yangu, iwe heri kwangu kwa ajili yako, na nafsi yangu iishi kwa ajili yako Basi ikawa Abramu alipofika Misri, Wamisri wakamwona huyo mwanamke ya kwamba yeye ni mzuri sana. Wakuu wa Farao wakamwona, nao wakamsifu kwa Farao; basi yule mwanamke akachukuliwa nyumbani mwa Farao. Naye akamtendea Abramu mema kwa ajili yake; naye alikuwa na kondoo na ng'ombe, na punda waume, na watumwa, na wajakazi, na punda wake, na ngamia.
Changamoto kubwa kwa Abrahamu sasa ni hofu, hofu ya kupoteza maisha kwaajili ya uzuri wa Sara mkewe, Abrahamu alitambua kuwa ana mke mzuri na kuwa hawezi kumkatalia Farao asimchukue bila kuuawa kwa hiyo alimweleza sara aseme kuwa yeye ni ndugu yake, na kwaajili ya hayo alifadhiliwa sana na Farao, na kupewa muzi, kondoo, punda na ngamia pamoja na watumwa na vijakazi utajiri wake ukaongezeka sana, na Ibrahimu alivipokea.

Watu wengi wanamlaumu sana Abrahamu kwa kosa hili, wanajiuliza kwanini Abrahamu alipokea mali hizi zote kana kwamba amemuuza Sara aidha kwa tendo hili inaonekana kana kwamba Abrahamu kama baba wa imani hapa alikosa kumuamini Mungu dhidi ya ulinzi wake kwake na mkewe, hivyo inaonekana kama Ibrahimu hapa amefanya swala la kipagani, vyovyote vile uonavyo ni lazima tukubali kuwa katika masiah haya kila mmoja wetu anaweza kukutana na changamoto ya aina Fulani na ukajikuta kuwa unapata ufumbuzi wa kibinadamu ambao kwa mtazamo wa wengine inaweza kuwa sio sahihi, chukulia mfano umeingiliwa na majambazi nyumbani na wanataka kumuua baba yako na mama yako, lakini wazazi wako wakawa wamejificha mahali na wewe unapajua lakini majambazi hawapajui na wanakuuliza wako wapi baba yako na mama yako tuwamalize tuwaue? Kwa sababu unajua kusema uongo ni dhambi je unaweza kuwaelekeza majambazi aliko baba yako na mama yako ili wawaue? Au mfano umekutana na mama amebeba mtoto na mtoto wake anaonekana ana sura mbaya sana lakini mama Yule na motto wake wanakuchekea kwa tabasamu zuri na unataka kumtia moyo mama yule je utamueleza kuwa mama hongera una mtoto ana uso mbaya kweli! Ni mara ngapi tu mewasifia watu kuwa wako vizuri na huku tunajua moyoni dhahiri kuwa hawako vizuri? Unaweza kuona sio kuwa tunajifunza uongo lakini tunajifunza kuwa yako mazingira ambayo kwa ubinadamu wetu hatuwezi kuchomoka kama unawekwa kwenye kona sawasawa, watu wengi wa Mungu makanisani ni wepesi sana kuhukumu na kuzogoma wanapoona makosa yaw engine na wakati mwingine wanakuwa na kimbelembele kushauri nini cha kufanya ilihali hawajui kuwa wewe unapitia mazingira ya namna gani, kwa bahati yako mazingira ambayo Mungu tu ndio anaweza kuelewa na kutujali, Tukio la Abrahamu hapa linaweza kuwa sio tukuio zuri wala lenye kuleta heshima au kuonyesha kujaa imani, ni tukio linaloonyesha mwanadamu akitafuta kujiokoa kwa njia zake lakini Mungu ndie hakimu wake na sio sisi! Kutokana na tukio hili Ibrahimu alimpoteza Sara na Sara alichukuliwa kuwa mke wa Farao.

Hata nikamtwaa kuwa mke wangu?


Hayoyote yalikuwa ni utangulizi tu kwangu, lakini hoja kubwa ambayo nilitaka wanafunzi wa Biblia tuweze kuidadavua kwa pamoja ni swala zima la kuchukuliwa kwa mke wa Ibrahimu Nyumbani kwa Farao ili kuwa mke wake swali kubwa hapa ni je farao alifanikiwa kumuingilia Sara kama mkewe? Kuna makundi makuu mawili ya mawazo ya wasomaji wa biblia kundi la kwanza wanaamini kuwa Sara alichukuliwa na Farao na huenda Farao alifanikiwa kumuingilia sara kama mke wake hii ni kutokna na uwazi wa biblia hapa na utofauti wa tukio kama hili kwa Abimeleki ona matukio haya

Mwanzo 12:18-20 “Ndipo Farao akamwita Abramu, akasema, N'nini hili ulilonitendea? Mbona hukuniambia ya kuwa huyo ni mkeo? Mbona ulisema, Huyo ni umbu langu, hata nikamtwaa kuwa mke wangu? Basi sasa, huyo mke wako umchukue, uende zako. Farao akawaagiza watu kwa ajili yake, wakampeleka njiani, na mkewe, na kila alichokuwa nacho.
 

      
Mwanzo 20:1-12 “Ibrahimu akaondoka huko kwenda nchi ya kusini, akakaa kati ya Kadeshi na Shuri, naye akatembea katika Gerari. Ibrahimu akamnena Sara mkewe, Huyu ni ndugu yangu. Basi Abimeleki mfalme wa Gerari akapeleka watu akamtwaa Sara. Lakini Mungu akamjia Abimeleki katika ndoto ya usiku, akamwambia, Umekuwa mfu wewe kwa sababu ya mwanamke huyu uliyemtwaa, maana ni mkewe mtu. Basi Abimeleki alikuwa hakumkaribia, akasema, Ee BWANA, Je! Utaua hata taifa lenye haki? Je! Hakuniambia mwenyewe, Huyu ni ndugu yangu? Na mwanamke mwenyewe naye alisema, Huyu ni ndugu yangu. Kwa ukamilifu wa moyo wangu, na kwa kuwa safi mikono yangu, nimefanya hivi. Mungu akamwambia katika ndoto, Nami nimejua ya kwamba kwa ukamilifu wa moyo wako umefanya hivi, ndipo nami nikakuzuia usinitendee dhambi, kwa hiyo sikukuacha umguse.Basi sasa umrudishe mwanamke kwa mtu huyo, maana yeye ni nabii, naye atakuombea, upate kuishi. Bali usipomrudisha, fahamu ya kwamba kwa hakika utakufa wewe na watu wote ulio nao. Abimeleki akaamka asubuhi na mapema, akawaita watumwa wake wote, akawaambia maneno hayo yote masikioni mwao, nao watu hao wakaogopa sana. Kisha Abimeleki akamwita Ibrahimu, akamwambia, Umetutenda nini? Nimekukosa nini, hata ukaleta juu yangu na juu ya ufalme wangu dhambi kuu? Umenitenda matendo yasiyotendeka. Abimeleki akamwambia Ibrahimu, Umeona nini hata ukatenda jambo hili? Ibrahimu akasema, Kwa sababu naliona, Yakini hapana hofu ya Mungu mahali hapa, nao wataniua kwa ajili ya mke wangu. Naye kweli ni ndugu yangu, binti wa baba yangu ila siye mwana wa mama yangu, ndipo akawa mke wangu.”

Sara anachukuliwa na farao na kufanywa kuwa mke wake na maandiko yako kimya kama endapo Farao alifanikiwa kumuingilia Sara au hapana, wakati katika kifungu cha Pili kabla Abimeleki hajamgusa Sara Mungu aliingilia kati na kumuonya kwa njia ya ndoto kwa aajili ya hayo wako wanaoamini kuwa Sara aliingiliwa na Farao, lakini Sara hakuguswa na Abimeleki! Kwa sababu ya lugha ile “hata nikamtwaa kuwa mke wangu” wengi wanaamini kuwa farao alimwingilia Sara, hoja zinajengwa kwamba hiki ndio kilikuwa kipimo kingine cha kuthibitisha kuwa sara alikuwa tasa, akiwa na miaka 65 hapa badomanaonekana kuwa mwanamke mzuri sana na wa kuvutia kiasi cha kuhatarisha maisha ya mumewe, Kama Sara angeshika mimba ya Farao ni wazi kuwa Abrahamu ndiye ambaye angejulikana kuwa ana tatizo, kwa hivyo wenghi wanaotetea hoja kuwa Farao alimuingilia Sara wanajaribu kutofautisha Lugha iliyotumika kwa Farao na ile iliyotumika kwa Abimeleki ikionyesha nkuwa Kuwa kule kwa Abimeleki Mungu aliingilia kati lakini kwa Farao Mungu aliachia Ibrahimu avune matunda ya uongo wake !

Mungu alumuhukumu Farao!


Binafsi sikubaliani na kundi la watu wanaofikiri kuwa Sara aliingiliwa na Farao, japo sihukumu mawazo yao lakini nataka kujenga hoja za kibiblia ili tuweze kuwa na uelewa mwema zaidi, kwanza ni muhimu kufahamu kuwa lugha ile Hata nikamtwaa kuwa mke wangu  katika tafasiri ya Biblia ya kiebrania kwa kiingereza ingeweza kusomeka namna hii “and i took her to me to wife” yaani kwa tafasiri nyepesi nilimchukua kwa kusudi la kuwa mke wangu, Ni muhimu kufahamu kuwa kabla farao hajamgusa tayari yeye na watu wake wote walipigwa na mapigo makubwa sana na inawezekana kupitia waonaji wake farao alitafuta sababu ya mapigo hayo mazitio huenda kupitia waganga au manabii wake na waonaji na wakamjulisha kuwa mapigo hayo yametoka kwa Mungu na ni kasababu amemtwaa mke wa mtu, na huenda Sara alikiri wazi kuwa yeye ni mke wa Abrahamu na sio ndugu, Farao alielewa kuwa mwanamke yule alikuwa ni mke wa mtu na alimrejesha haraka na kumuondoa katika inchi yake, Kwa kawaida kulinga na mila na desturi za kale mwanamke alipochukuliwa awe mke wa mtu au mfalme hakuwa anapelekwa moja kwa moja siku hiyo hiyo bali aliwekwa kwenye Haremu yaani jumba la kifalme na kuanza kuandaliwa unaweza kuona Esta 2:12 “Basi ilipowadia zamu yake mwanamwali mmojawapo aingie kwa mfalme Ahasuero, hali akiisha kufanyiwa sawasawa na sheria ya wanawake miezi kumi na miwili; yaani, ndivyo zilivyotimia siku zao za utakaso, miezi sita kwa mafuta ya manemane, na miezi sita kwa manukato na vifaa vya utakaso wa wanawake;” unaona kwa hivyo kulikuwa na muda maalumu wa maandalizi kabla mwanamke huyo kupelekwa kwa mfalme kulikuwa na miezi ya uangalizi kama miezi 12 kabla ya mke maalumu hii ilikuwa ni kwa sababu mbalimbali za kiusalama, taratibu na kuwalinda wafalme na magonjwa na kadhalika kwa hiyo kwa Sara huenda pia alikuwa yuko katika maandalizi, kwa hivyo kumrejesha kwa mumewe lilikuwa tendo la haki lilolofanya na Farao.

Pamoja na hayo pia maandiko yanathibitisha wazi kuwa Mungu aliingilia kati biola kujali madhaifu yao ya kibinadamu lakini kwaajili ya agano lake aliwaadhibu wenye mamlaka ili wasiwaonee wapakwa mafuta wake ona Zaburi 105:14-15 “Hakumwacha mtu awaonee, Hata wafalme aliwakemea kwa ajili yao. Akisema, Msiwaguse masihi wangu, Wala msiwadhuru nabii zangu.Kwa hiyo kwa mujibu wa maandiko ni wazi kuwa Sara hakuguswa na mwisho wa siku Farao alimrejesha Sara kwa Abrahamu kama Abimeleki alivyofanya pia, farao alihakikisha kuwa Abrahamu anakuwa saklama ana anaondoka Misri mara moja, Licha ya kuwepo kwa udhaifu wa Abrahamu Mungu ni mwingi wa rehema alitimiza ahadi yake kwa Abrahamu na Abrahamu aliondoka akiwa na ulinzi na mali nyingi bika kukaa sana Misri

Tukio hili linaweza kuwa funzo kwetu kwamba wakati mwingine Mungu anaweza kuruhusu mabaya yakatupata au yakampata mtu katika mazingira Fulani kwa kusudi la kutokeza mema Faraoa lipigwa mapigo makubwa sana ambayo yalipelekea atende wema huku akigundua kuwa yuko Mungu aliye hai, kila jambo linalotutokea katika maisha yetu lina makusudi yake, katika maisha yetu Yeremia 29:11 “Maana nayajua mawazo ninayowawazia ninyi, asema Bwana, ni mawazo ya amani wala si ya mabaya, kuwapa ninyi tumaini siku zenu za mwisho”.  Mungu wakati wote anatuwazia mema ingawa Abrahamu alitegemea kuokolewa kwa akili zake na ujanja wake alikamatwa kwa uongo wake lakini Mungu alithibitisha nguvu zake na kuonyesha kuwa ni yeye pekee mwenye uwezo wa kuokoa, Mungu anakusudi kwa kila jambo hata mateso, Mapenzi yake yatatimizwa na jina lake litatukuzwa tu


Na Rev. Innocent Kamote

Mkuu wa wajenzi mwenye hekima!

0718990796/0784394550
ikamote@yahoo.com

Alhamisi, 11 Juni 2020

Mama yangu alinichukua Mimba hatiani!


Zaburi 51:5 “Tazama, mimi naliumbwa katika hali ya uovu; Mama yangu alinichukua mimba hatiani



Utangulizi:


Ni muhimu kufahamu kwamba Mojawapo ya Maandiko ambayo yamekuwa na changamoto kubwa sana kwa wasomi wengi wa Biblia na kukutana na ugumu katika tafasiri zake ni Pamoja na andiko hili katika Zaburi 51:5 “Tazama, mimi naliumbwa katika hali ya uovu; Mama yangu alinichukua mimba hatianiwote tunajua wazi kuwa zaburi hii imeandikwa na Daudi, na maneno yake ni sehemu ya toba aliyokuwa akiifanya baada ya kufanya dhambi, ya zinaa na mke wa Huria na kufanya njama ya mauaji dhidi ya Uria ili kuficha ushahidi, ni baada ya kukabiliwa na Nabii  Nathan na kuonywa kuhusu kosa lake Daudi alitubu na kusema maneno haya yaliyopo katika zaburi ya 51.  Kuna maneno mengi sana aliyasema katika zaburi hii kama sehemu ya toba yake lakini neno kuu na ambalo linazua mjadala mkubwa sana kwa wasomi wengi wa Biblia ni maneno haya “MAMA YANGU ALINICHUKUA MIMBA HATIANI!”  Swali kubwa likiwa ni kwanini Daudi anazungumza maneno haya? Anamaanisha nini, Daudi anazungumzia hali ya mwanadamu kuzaliwa akiwa na asili ya dhambi? Au anamaanisha kuwa mwanadamu anaanza kuwa mwenye dhambi tangu siku mimba inapotungwa? Lakini pia inaweza kumaanisha kuwa Daudi aliamini kuwa mama yake alimzaa katika hali ya dhambi?


Kumbuka maneno haya- “Hatiani” Kama ilivyoaminika katika jamii yake kuwa mama yake alimzaa mtoto huyo kutokana na zinaa. Maandiko haya yenye uzito mkubwa na majonzi makubwa yanatusaidia kuelewa kitu fulani na kingine cha ziada katika maisha na mapito ya Daudi ambacho kinaweza vilevile kuhuisha maisha yetu kwa upya, Kwa msingi huo leo tutachukua muda kuweza kufanya uchunguzi wa kina sana na wa ndani zaidi kuhusu utata wa andiko hili na maana zake kwa kadiri ya mawazo mbalimbali ya wasomi wa Biblia na kwa kadiri ya neema kwa msaada wa Roho Mtakatifu mwalimu mkuu;-


Nani mwandishi wa Zaburi hii?


Ili andiko hili liweze kutafasirika vema jambo la kwanza ni lazima tuwe na uhakika wa mwandishi wa Zaburi hii, Mfano kama Zaburi hii imeandikwa na Sulemani na Sulemani labda ndiye aliyekuwa anatubu hapa kwa sababu zaburi hii ni zaburi ya toba ni zaburi ya kuomba rehema kwa Mungu unaweza kuona inavyoanza katika mstari ule wa kwanza hivi;- 

Zaburi 51:1-2 “Ee Mungu, unirehemu, Sawasawa na fadhili zako. Kiasi cha wingi wa rehema zako, Uyafute makosa yangu. Unioshe kabisa na uovu wangu, Unitakase dhambi zangu.” 

Ni wazi kuwa mstari wa tano ungeweza kufikiriwa kuwa labda Sulemani anakumbuka historia ya kuzaliwa kwake, kupitia makosa ya Daudi kwa mama wa Sulemani ambaye ni Bathsheba mke wa Uria, Lakini maandiko yako wazi kuwa Bathsheba siye aliyekosea yeye alikosewa na adhabu ya Mungu ilianguka kwa mtoto wa kwanza ambaye Daudi alizaa na Bathsheba na ambaye alifariki mapema kama njia ya kutiwa nidhamu na Mungu, 

2Samuel 12:14 “Lakini, kwa kuwa kwa tendo hili umewapa adui za Bwana nafasi kubwa ya kukufuru, mtoto atakayezaliwa kwako hakika yake atakufa. 

na kwa vile Uria aliyekuwa mume wa Bathsheba alikuwa amekwisha kuawa, na maandiko yako wazi kuwa Daudi alikuwa amemchukua Bathsheba kama mke wake sasa basi Sulemani anazaliwa kama mtoto halali wa Daudi kwa Bathsheba akitambuliwa na maandiko namna hii 

Mathayo 1:6 “Yese akamzaa mfalme Daudi. Daudi akamzaa Sulemani kwa yule mke wa Uria;” 

kimsingi hapa kosa lilikuwa la Daudi kuliko Bathsheba (japo wote wlifanya dhambi) na kama Zaburi hii ingekuwa ya Sulemani basi Mstari wa tano ungepaswa kusomaeka “Baba yangu alinitungisha mimba Hatiani” tukinena kiwazimu! Kwa msingi huo kwa namna fulani hatuoni wazi kuwa toba hii ni ya Sulemani, Lakini wote tunakubaliana wazi kuwa uchunguzi wa kimaandiko unaonyesha wazi kuwa zaburi hii ni miongoni mwa zaburi za toba na ni wazi kuwa iliandikwa na Daudi kwa kusudi la kutubia dhambi yake aliyoifanya kwa kumuingilia Mke wa Uria na pia kula njama za kumuua Uria na toba hii ilifanyika baada ya kukabiliwa na nabii Nathan ili Daudi arejee katika uhusiano wake na Mungu, Na kama hivyo ndivyo basi swala la msingi linabaki pale pale kwamba zaburi hii ni ya Daudi na maneno hayo ni toba ya Daudi na sio Sulemani, Sasa basi maneno yale “Mama yangu alinichukua Mimba hatiani!”  yana maana gani? Kwanini Daudi anayasema maneno hayo je alikuwa amamaanisha nini Hapa ziko dhana mbalimbali kuhusu maneno hayo:-


Mama yangu alinichukua Mimba hatiani!


1.       Mtazamo wa wayahudi: Kwa mujibu wa masimulizi ya Marabi, na maandishi ya kihistoria ya kiyahudi na tamaduni zao inaaminika kuwa maneno haya yalikuwa yakimaanisha kuwa Daudi alizaliwa nje ya ndoa yaani mama yake Daudi aliyeitwa NIZBETH alifanya zinaa kumpata mtoto huyo, swala hili liliaminika hivyo miongoni mwa Familia ya Yese, akiwemo Yese mwenyewe na kaka zake Daudi. Kwa hivyo kulikuweko na imani kwamba Daudi ni mwana wa haramu na wala sio mwana wa halali wa mzee Yese ona Zaburi 69:7-8 “Maana kwa ajili yako nimestahimili laumu, Fedheha imenifunika uso wangu. Nimekuwa mgeni kwa ndugu zangu, Na msikwao kwa wana wa mama yangu.” Maneno haya nimekuwa mgeni kwa ndugu zangu, kwa kiingereza “Stranger” katika Lugha ya kiibrania yanasomeka “MUZAR” yaani kwa kiingereza “Bastard” yaani mtoto asiye safi, mwana haramu!,  na neno lingine “Msikwao” kwa kiingereza “Alien” asiyetambulika yaani mwana wa mashaka, mgeni au mkimbizi, Kimsingi zaburi ya 69 kwa mujibu wa wanazuoni wa kiyahudi ni zaburi ya Daudi aliyoandika wakati wa maisha yake ya mapema akiwa kijana ikionyesha kuwa kijana huyu alikuwa na maumivu makali moyoni yanayotokana na mateso na kukataliwa kabisa, na ndugu zake wakiamini kuwa ni mwana wa haramu, na alichukiwa sana akihesabika kama sababu ya kusambaratika kwa familia na kudharaulika kwa mama yao. Zaburi ya 69 inafunua aina ya maisha magumu sana aliyopitia Daudi ya kukataliwa na kunyanyapaliwa na kudharauliwa na kila mtu aliyemuona inasemekana kuwa wakati wa maisha yake ya utotoni hadi ukubwani hakuwa na rafiki hata mmoja wa kumtia moyo alikuwa mtu wa kulaumiwa, kuaibishwa na kufedheheshwa tu, 

   Zaburi 69:19-20 “Wewe umejua kulaumiwa kwangu, Na kuaibika na kufedheheka kwangu, Mbele zako Wewe wako watesi wangu wote. Laumu imenivunja moyo, Nami ninaugua sana. Nikangoja aje wa kunihurumia, wala hakuna; Na wa kunifariji, wala sikumwona mtu”.Zaburi hii ya 69 ilikuwa ni sauti ya mtu aliyeteseka mno, akidhalilishwa na kuaibishwa, Daudi alikuwa amezungukwa na Maadui wa ndani na nje katika jamii yake na wengi wakiwaza kumuua na wakati mwingine kitu kilipopotea alisingiziwa yeye na alilipishwa kwa nguvu ona  habari zake Zaburi 69:4 “Wanaonichukia bure ni wengi Kuliko nywele za kichwa changu. Watakao kunikatilia mbali wamekuwa hodari, Adui zangu kwa sababu isiyo kweli. Hata mimi nalilipishwa kwa nguvu Vitu nisivyovichukua.Hiki kilikuwa kipindi kigumu sana katika maisha ya Daudi Zaburi ya 69 ni sauti ya mtu aliyelemewa na mzigo mzito sana na ni maombi ya ukombozi dhidi ya maisha ya mateso na Daudi inasemekana anayazungumza haya katika kipindi cha miaka 20-28 hivi cha maisha yake yaliyojawa na utata mwingi na kugubikwa na huzuni na kukataliwa.


Je nini sababu kubwa ya mateso haya ya Daudi nyumbani kwao?


Daudi alizaliwa katika familia ya Mzee Yese, Wayahudi wenyewe wanamuita Yishai, Mzee huyu alikuwa miongozi mwa wazee sabini waliokuwa wafanya sheria na waamuzi wa sheria za kiyahudi “Sanhedrin” yaani mahakama kuu ya Wayahudi, na alikuwa ni mtu aliyejipatia umaarufu mkubwa sana katika kizazi chake na katika mji wao Bethelehemu, inasemekana kuwa alikuwa mtu wa haki kiasi ambacho TALMUD (Shabbat 55b) imenukuu kuwa “Yese alikuwa mtu mwenye haki kiasi ambacho hakustahili kifo isipokuwa kwa sababu ya tatizo la Nyoka tu” yaani alikufa kwa sababu ya tatizo la Bustani ya Eden tu na tamko la Mungu kwa  Adam na Eva  kuwa watakufa siku watakapokula matunda waliyokatazwa, inasemekana kuwa hakuna dhambi wala hatia iliyowahi kuonekana ndani ya Mzee Yese.


Hata hivyo kulikuwa na tatizo moja kubwa sana katika familia ya Yese na hili ndilo lilopelekea Daudi kusema yeye amekuwa kama Mgeni kwa ndugu zake, Daudi hakuruhusiwa kula pamoja na familia yake, yeye aliwekewa chakula chake pembeni sana, alipewa kazi ngumu ya kuchunga kondoo sehemu yenye wanyama wakali kama Simba na Dubu ili yamkini ikiwezekana afie huko, Kwa hiyo Maisha ya Daudi ya ujanani yalikuwa maisha magumu mno na ni mtu mmoja tu aliyekuwa akiumizwa na maisha ya Daudi ambaye ni mama yake tu ambaye kukataliwa kwa mwanaye kulimjumuisha na yeye hata hivyo naye hakuwa na nguvu ya kuzuia kile alichotendewa yeye na mwanaye!, Daudi alihesabika kama mdudu tu na hakuna mtu alimhesabu kuwa kitu, alilaumiwa na watu na kufanyiwa dhihaka, kufyonywa na kuchekwa ona Zaburi 22:6-7 “Lakini mimi ni mdudu wala si mtu, Laumu ya wanadamu na mzaha wa watu. Wote wanionao hunicheka sana, Hunifyonya, wakitikisa vichwa vyao;” ukweli ni kuwa Daudi na mama yake Nizbeth walikuwa wakimuomba na kumsubiria Mungu awasaidie tu katika hali waliyokuwa wakiipitia wakati huu bado ilionekana kana kwamba Mungu amewaacha walikuwa wakimsubiria Mungu awaokoe na ukatili wa kifamilia uliokuwa ukiwakabili Zaburi 22:1-5 “Mungu wangu, Mungu wangu, Mbona umeniacha? Mbona U mbali na wokovu wangu, Na maneno ya kuugua kwangu?  Ee Mungu wangu, nalia mchana lakini hujibu Na wakati wa usiku lakini sipati raha. Na Wewe U Mtakatifu, Uketiye juu ya sifa za Israeli. Baba zetu walikutumaini Wewe, Walitumaini, na Wewe ukawaokoa. Walikulilia Wewe wakaokoka, Walikutumaini wasiaibike.Haya yalikuwa maisha ya Daudi


NIZBETH ni nani hasa? Mwanamke huyu ni moja ya wanawake muhimu sana katika historia ya wayahudi, japo hatajwi katika maandiko lakini waebrania wanamuita Nitzevet Adael, kwa mujibu wa kitabu cha masimulizi ya Kiyahudi TALMUD mwanamke huyu ndie mama wa Mfalme Daudi na alikuwa na watoto tisa na wote alizaa na mzee Yese, watoto hao ni Eliabu, Abinadab, Shama, Nethaneel, Raddai, Ozem, Daudi, Seruiah na Abigaili.


Kwa mujibu wa masimulizi hayo ya kiyahudi ni Kwamba Mzee Yese ambaye wayahudi wanamuita Yishai  alikuwa ni mjukuu wa Boaz na Ruthu, baada ya miaka mingi sana ya ndoa yake yeye na Nizbeth na baada ya kuzaa watoto wa kiume kadhaa kabla ya kuzaliwa Daudi Mzee Yese alianza kuwa na mashaka kuhusu uzao wake hasa kwa sababu ya historia ya babu yake Boazi na Bibi yake Ruthu, kwamba ingawa Ruthu alikuwa amemuamini Mungu wa Israel lakini Ruthu alikuwa mmoabu hivyo kulikuwa na mashaka kama watoto waliozaliwa na huyu mmoabu wana haki ya kumtumikia Mungu wa Israel kama wayahudi wa asili? Japo Yese alikuwa mtu mkubwa lakini tafasiri za Torati kati yake na wenzake ziliwapa mashaka makubwa sana kama wajukuu wa Boazi yeye na wanawe wanaweza kuwa wenye kufaa kwa utumishi wa Mungu na utawala au ufanya sheria, hii ni kwa sababu wakati wana wa Israel wanatoka Misri wamoabu walisimama kikatili kinyume na Israel ili wasipite katika nchi yao na hivyo torati ya Musa ilikataza kabisa wana wa Israel wasioane na wamoabu ona::-


Kumbukumbu la Torati 23:2-3 “Mwana wa haramu asiingie katika mkutano wa Bwana; hata kizazi cha kumi asiingie aliye wake katika mkutano wa Bwana. Mwamoni wala Mmoabi wasiingie katika mkutano wa Bwana; wala hata kizazi cha kumi mtu wao asiingie katika mkutano wa Bwana milele;


Biblia ya kiingereza NIV inasomeka vema zaidi katika mistari hii Deuteronomy 23:2-3 “No one born of a FORBIDDEN MARRIAGE nor any of his descendants may enter the assembly of the LORD, even down to the tenth generation, No Ammonite or Moabite or any of his descendants may enter the assembly of The LORD even down to the tenth generation.


Kwa mujibu wa masimulizi ya Kiyahudi Boazi alipomuoa Ruthu alikuwa ni mfanya sheria na alikuwa na ufahamu kuhusu Sheria hii na labda angepata muda wa kufafanua kwa jamii kwa nini alioa mwanamke mmoabu na torati ilikataza? Je mwanaume akimuoa mwanamke wa Moabu ambaye amemuamini Mungu wa Israel je wanawe wataweza kuwa halali kuingia katika mkutano wa Bwana? Bahati mbaya inasemekana kuwa Boazi baada ya kumuoa Ruthu alikufa mara moja akimuacha mja mzito na kumzaa Obedi, Obedi yeye alimtumikia Mungu kwa Heshima kubwa na jina lake Obedi maana yake ni Mtumishi wa Mungu aliishi maisha ya haki sana na kuwa na heshima kubwa katika jamii jambo lililofanya akubalike katika jamii bila kujali kuwa mama yake alikuwa mmoabu, Hali kadhalika mwanaye yaani Yese naye aliishi maisha ya haki sana kiasi cha kukubalika na jamii ya Israel kuwa ni mwenye kufaa na watoto wake pia, hata hivyo  wakati wa maisha ya Yese kuliibuka mijadala mikubwa sana kuhusu Sheria ya Musa kwamba Israel wasioane na wamoabu na kuwa wamoabu wasiingie katika mkutano wa Bwana milele jambo hili lilimpa wasiwasi mkubwa sana Yese, jamii yake iliona kuwa Yese mwenye Damu ya kimoabu toka kwa bibi yake Ruthu na hata watoto wake wasingeweza tena kwa namna yoyote kuwa wenye kufaa kwa vile walijulikana kuwa na damu ya kimoabu kwa hivyo wametokana na ndoa zilizokatazwa na Torati ya Musa unaweza kuona! ushahidi wa maisha ya Daudi wakati wa mapambano na Sauli unathibitisha kwamba Daudi aliwakimbiza wazazi wake kwa mfalme wa Moabu ona 1Samuel 22:3-4 “Basi Daudi akaondoka huko, akakimbilia pango la Adulamu; na ndugu zake na watu wote wa mbari ya baba yake waliposikia habari hiyo, wakamwendea huko. Na kila mtu aliyekuwa katika hali ya dhiki, na kila mtu aliyekuwa na deni, na watu wote wenye uchungu mioyoni mwao, wakakusanyika kwake; naye akawa jemadari wao; nao waliokuwa pamoja naye walipata kama watu mia nne. Kutoka huko Daudi akaenda Mispa ya Moabu; akamwambia mfalme wa Moabu, Tafadhali ukubali baba yangu na mama yangu watoke huko waliko, wakakae kwenu, hata nitakapojua Mungu atakalotenda kwa ajili yangu.  Akawaleta mbele ya mfalme wa Moabu, nao wakakaa pamoja naye wakati wote Daudi alipokuwa ngomeni.Inasemekana moja ya sababu ya familia hii ya Yese kwenda kujificha huko Moabu ni kwa sababu ya uhusiano wa Bibi yao Ruthu aliyetokea katika nchi ya Moabu


Kutokana na kuweko kwa mkanganyiko huo kuwa wayahudi wenye damu ya kimoabu wanafaa kuoana na wayahudi halisi au la? Yese na wanawe ni Wayahudi wenye asili ya kimoabu kutokana na babu yao Boazi kumuoa Ruth  aliyekuwa mwongofu wa kiyahudi kutoka moabu na mke wa Yese, Nizbeth alikuwa myahudi halisi wakati huu akiwa na watoto saba wa kiume na wawili wa kike, Daudi akiwa hajazaliwa wazee wa mji walimuamuru Yese aachane na Nizbeth na wala wasigusane tena!  Na kusiweko uhusiano tena kati ya Yese na Nizbeth, Hivyo familia ilikubaliana kuwa Yese na Nizbeth kuwa waachane (na kwa vile haukuwa ugomvi) waliachana katika hali ya upendo tu kwamba Nizbeth ambaye ni myahudi halisi asitende dhambi na myahudi mwenye damu ya kimoabu kwa hivyo Yese aliahidi kuwa atamtuza Nizbeth na kumlisha isipokuwa tu hakutakuwa na uhusiano wa kindoa ili kutunza heshima zao katika jamii!, watoto wote wakubwa wa Yese walifahamu utengano huo na walikubaliana. Jambo hili lilikubalika na Wazee ambao waliitwa “WAKETIO LANGONI” waketio langoni walikuwa ni wazee wa mji wenye kuheshimika kwa kufanya maamuzi ya kimahakama ona mfano Ruthu 4:1-12 “Basi Boazi akakwea kwenda mpaka langoni, akaketi pale; na tazama, yule mtu wa jamaa aliyekuwa karibu, ambaye Boazi amemnena, akapita. Naye akamwita, Haya! Wewe, karibu, uketi hapa. Naye akaja akaketi. Kisha akatwaa watu kumi miongoni mwa wazee wa mji, akawaambia, Ninyi nanyi, ketini hapa. Wakaketi. Kisha akamwambia yule jamaa, Huyu Naomi, aliyerudi hapa kutoka nchi ya Moabu, anauza sehemu ya ardhi aliyokuwa nayo ndugu yetu, Elimeleki; nami ilikuwa nia yangu nikujulishe wewe, na kukuambia, Uinunue mbele ya hawa waliopo na mbele ya wazee wa watu wangu. Kama wewe utaikomboa, haya, uikomboe; lakini kama hutaikomboa, uniambie ili nijue mimi; kwa kuwa hakuna mtu wa kuikomboa ila wewe, na baada yako ni mimi. Naye akasema, Nitaikomboa mimi.  Ndipo Boazi aliposema, Siku ile utakapolinunua shamba mkononi mwa Naomi, unamnunua Ruthu pia, huyu Mmoabi, mkewe marehemu, ili makusudi umwinulie marehemu jina katika urithi wake. Basi yule jamaa aliyekuwa wa karibu akasema, Mimi sitaweza kulikomboa kwa nafsi yangu, nisije nikauharibu urithi wangu mwenyewe; basi haki yangu ya kulikomboa ujichukulie wewe, maana mimi sitaweza kulikomboa. Basi hii ilikuwa desturi zamani za kale katika Israeli, kwa habari ya kukomboa na kubadiliana, ili kuyahakikisha yote; mtu huvua kiatu chake na kumpa mwenziwe; ndivyo walivyohakikisha neno katika Israeli. Basi yule jamaa akamwambia Boazi, Wewe ujinunulie mwenyewe. Akavua kiatu chake. Naye Boazi akawaambia wale wazee na watu wote, Leo hivi ninyi ni mashahidi ya kwamba mimi nimenunua yote yaliyokuwa ya Elimeleki, na yote yaliyokuwa ya Kilioni na Maloni, mkononi mwa Naomi. Tena, huyu Ruthu Mmoabi, mkewe Maloni, nimemnunua awe mke wangu, makusudi nipate kumwinulia marehemu jina katika urithi wake, jina lake marehemu lisikatike miongoni mwa ndugu zake, wala langoni pa mji wake; leo hivi ninyi ni mashahidi.  Na watu wote waliokuwapo langoni, na wale wazee, wakasema, Naam, sisi ni mashahidi. Bwana na amfanye mwanamke huyu aingiaye nyumbani mwako kuwa kama Raheli na kama Lea, wale wawili walioijenga nyumba ya Israeli. Nawe ufanikiwe katika Efrata, na kuwa mashuhuri katika Bethlehemu. Nyumba yako na ifanane na nyumba yake Peresi, ambaye kwamba Tamari alimzalia Yuda, kwa wazao atakaokupa Bwana katika mwanamke huyu.” Unaona waketio Langoni walikuwa ni wazee wenye ujuzi wa torati waamuzi na ndio waliokuwa wakifanya maamuzi, kwa hiyo Langoni ilikuwa ni kama mahakamani, Hapo walipitisha kuwa Boazi amnunue Ruthu na kuwa mkewe kama jamaa aliye karibu, lakini kumbuka baadaye wazee waliokuweko katika kizazi za Yese ndio walioamua Yese aachane na Nizbeth na ndio vilevile walikuwa miongoni mwa watu waliomuona Daudi kama mtoto asiyefaa nao walishiriki kumsema vibaya ona Zaburi 69:10-12 “Nilipolia na kuiadhibu roho yangu kwa kufunga, Ikawa laumu juu yangu. Nilipofanya gunia kuwa nguo zangu, Nikawa mithali kwao. Waketio langoni hunisema, Na nyimbo za walevi hunidhihaki.Mtazamo wa wazee hao ilikuwa Yese na wanawe ingawa ni wema lakini wamezaliwa katika ndoa zilizokatazwa na torati ya Musa!


Baada ya miaka kadhaa kupita Yese alitamani tena kuwa na mtoto ambaye hatakuwa na maswali kuhusu asili yake kwamba asiwe mwamoni wala mmoabu, hivyo aliazimia kuanzisha uhusiano na mjakazi wa Nizbeth ambaye alikuwa mkanaani, Yese alimwambia mjakazi huyo maneno haya  “Kama nitakubalika kama Myahudi halali basi wewe utafaa kuwa mke halali uliyemuamini Mungu wa Israel kwa hiyo utaweza kunizalia mtoto halali asiye na lawama kwa vile haikubaliki kwa mtu mwenye damu ya mmoabu au mwamoni kuzaa na myahudi hivyo utakuwa huru wala hutakuwa mtumwa tena” Mjakazi huyo wa Nizbeth alielewa mpango huu wa Yese na alimueleza Nizbeth kwa vile alikuwa mwaminifu sana kwa bibi yake, Nizbeth alikuwa anapitia uchungu mkubwa sana wa kukaa hivihivi akiwa ametengwa na mumewe hivyo walikubaliana na mjakazi wake  kwamba usiku ule Yese atakapotaka kuingia kwako tafadhali uniache niingie mie kama Leah alivyofanyiwa na Raheli na mjakazi alikubali ombi la Nizbeth huku Yese akiwa hajui mpango huo, Nizbeth aliingia na kulala na mumewe na kwa bahati njema alipata ujauzito alitoka asubuhi na mapema kama ilivyo desturi za wakati huo na Yese hakujua kuwa alilala na mkewe halali Nizbeth (Ilikuwa desturi zamani katika jamii ya kiyahudi mwanamke kumuendea mwanaume wakati wa usiku na kuondoka asubuhi baada ya kumhudumia kwa tendo la ndoa) ona Ruthu3:1-14 “Kisha Naomi akamwambia mkwewe, Je! Mwanangu, si vizuri nikutafutie raha, ili upate mema? Basi na huyu Boazi, je! Siye wa mbari yetu, ambaye ulikuwapo pamoja na wasichana wake? Tazama, usiku wa leo atakuwa akipepeta shayiri pale ugani. Basi wewe oga, ujipake mafuta ujivike mavazi yako, kisha uende kwenye uga; walakini usijionyeshe kwake mtu yule, ila atakapokwisha kula na kunywa. Nayo itakuwa wakati atakapolala, utapaangalia mahali alalapo, nawe uingie, uifunue miguu yake ujilaze hapo; na yeye atakuambia utakalofanya. Akamwambia, Hayo yote unenayo mimi nitayafanya. Basi akashuka mpaka ugani; akafanya yote kama vile mkwewe alivyomwagiza. Ikawa huyo Boazi alipokwisha kula na kunywa, na moyo wake umekunjuka, alikwenda kulala penye mwisho wa chungu ya nafaka; na huyo mwanamke akaja taratibu, akaifunua miguu yake, akajilaza papo hapo. Na ikawa usiku wa manane yule mtu akasituka, akajigeuza; na kumbe! Yupo mwanamke amelala miguuni pake. Akasema, Ama! Ni nani wewe? Akamjibu, Ni mimi, Ruthu, mjakazi wako; uitande nguo yako juu ya mjakazi wako; kwa kuwa ndiwe wa jamaa aliye karibu. Akamwambia, Mwanangu, ubarikiwe na Bwana; umezidi kuonyesha fadhili zako mwisho kuliko mwanzo, kwa vile usivyowafuata vijana, kama ni maskini kama ni matajiri. Basi, mwanangu, usiogope; mimi nitakufanyia yote uyanenayo; kwa maana mji wote pia wa watu wangu wanakujua ya kwamba u mwanamke mwema.  Tena ndiyo kweli ya kuwa mimi ni wa jamaa yako aliye karibu; lakini kuna mtu wa jamaa aliye karibu kuliko mimi. Wewe ungoje usiku huu; kisha, asubuhi, kama akikubali kukufanyia impasavyo jamaa, haya, na akufanyie; lakini ikiwa hataki yeye, basi mimi nitakufanyia impasavyo jamaa; Bwana aishivyo. Ulale wewe hata asubuhi. Hivyo huyo mwanamke akalala miguuni pake hata asubuhi; akaondoka mapema asijaweza mtu kumtambua mwenziwe; maana Boazi amesema, Isijulikane kabisa ya kuwa mwanamke alifika penye uga.” Unaona kwa mujibu wa mila hii, Nizbeth alikwenda kulala na mumewe  na kuondoka asubuhi bila Yese kujua.


Baada ya miezi kama mitatu hivi ilibainika kuwa Nizbeth ana mimba, boma zima lilifahamu na watoto wake wakubwa walijua na mzee Yese pia alitambua kuwa Nizbeth ana mimba boma zima walikusudia apigwe mawe afe kwa sababu huenda mimba hiyo ameipata kwa uzinzi, Nizbeth hakutaka kabisa kuelezea namna alivyopata mimba hiyo kwa sababu alijua Yese atafadhaika sana na hakutaka kumuudhi, Nizbeth aliamua atakaa kimya tu! Aliweka nadhiri ya kukaa kimya mpaka Mungu mwenyewe alete haki, Yese akiwa hajui kabisa kuwa mimba hiyo imetokea vipi aliwaamuru watoto wake wasimuue Nizbeth wamuache aishi, lakini mtoto atakayezaliwa na ahesabike kama mtumwa tu na mwana wa haramu! Na asiruhusiwe kuoa Myahudi.


Tangu wakati huu hiki ndio kikawa chanzo kikubwa zaidi cha chuki dhidi ya Nizbeth na mwanaye Daudi, walichukiwa na jamii na kuhesabika kama watu wasiofaa na walioleta aibu kubwa sana katika familia ya Yese! Kijana huyu alianza kupitia maisha magumu na ya kukataliwa na jamii akihesabika kama mwana wa zinaa na mtoto wa dhambi!  Na mtumwa.  Alipelekwa kuchunga kondoo na kutokuhesabika kama sehemu ya familia ya Yese, habari zilienea Bethelehemu yote, na kama kitu kuilipotea alisingiziwa yeye na hata kulipishwa! Watu walisema mambo yote mema ya Boazi yamejulikana kwa Mwanae Yese na watoto wake saba lakini mambo mabaya ya kuoa Mmoabu ya Ruthu yamejulikana kupitia mtoto huyu mlaaniwa! Na ndio maana Daudi alikuwa akikaripiwa na nduguze na kuhesabika kama motto mwenye kiburi na anayestahili kushinda porini tu akiwachunga kondoo ona 1Samuel 17:12-28 “Basi Daudi alikuwa mwana wa yule Mwefrathi, wa Bethlehemu ya Yuda, aliyeitwa jina lake Yese; naye huyo alikuwa na wana wanane; na yeye mwenyewe alikuwa mzee siku za Sauli, na mkongwe miongoni mwa watu. Nao wale wana watatu wa Yese waliokuwa wakubwa walikuwa wamefuatana na Sauli kwenda vitani, na majina ya hao wanawe watatu waliokwenda vitani ni haya, mzaliwa wa kwanza Eliabu, na wa pili wake Abinadabu, na wa tatu Shama. Naye huyo Daudi alikuwa mdogo wa wote; na hao watatu waliokuwa wakubwa wakafuatana na Sauli.Basi Daudi alikuwa akienda kwa Sauli na kurudi ili awalishe kondoo za baba yake huko Bethlehemu.Naye yule Mfilisti hukaribia asubuhi na jioni, akajitokeza siku arobaini. Ndipo Yese akamwambia Daudi mwanawe, Haya! Sasa uwachukulie ndugu zako efa ya bisi, na mikate hii kumi, ipeleke upesi kambini kwa ndugu zako; ukampelekee akida wa elfu yao jibini hizi kumi, ukawaangalie, wa hali gani, kisha uniletee jawabu yao. Basi Sauli, na watu wote wa Israeli, walikuwa katika bonde la Ela, wakipigana na Wafilisti. Daudi akaondoka asubuhi na mapema, akawaacha kondoo pamoja na mchungaji, akavitwaa vitu vile, akaenda, kama Yese alivyomwamuru; akafika penye magari, wakati lile jeshi walipokuwa wakitoka kwenda kupigana, wakipiga kelele za vita. Nao Waisraeli na Wafilisti wakajipanga, jeshi hili likikabili jeshi hili. Basi Daudi akaviacha vile vyombo vyake katika mkono wa mlinda vyombo, akalikimbilia jeshi, akafika, akawasalimu ndugu zake. Hata alipokuwa akisema nao, kumbe! Yule shujaa alitokea, yule Mfilisti wa Gathi, jina lake Goliathi, akitoka katika jeshi la Wafilisti, akasema maneno yale yale; naye Daudi akayasikia. Na watu wote wa Israeli walipomwona yule mtu wakakimbia, wakaogopa sana. Watu wa Israeli wakasema, Je! Mmemwona mtu huyu aliyepanda huko? Hakika ametokea ili awatukane Israeli; basi, itakuwa, mtu yule atakayemwua, mfalme atamtajirisha kwa utajiri mwingi, naye atamwoza binti yake, na kuifanya mbari ya baba yake kuwa huru katika Israeli. Daudi akaongea na watu waliosimama karibu, akisema, Je! Atafanyiwaje yeye atakayemwua Mfilisti huyo, na kuwaondolea Israeli aibu hii? Maana Mfilisti huyu asiyetahiriwa ni nani hata awatukane majeshi ya Mungu aliye hai? Nao watu wakamjibu vivyo hivyo, wakisema, Ndivyo atakavyofanyiwa mtu yule atakayemwua. Naye Eliabu, mkubwa wake, alisikia hapo alipoongea na watu; na hasira yake Eliabu ikawaka juu ya Daudi, akasema, Mbona wewe umeshuka hapa? Na kondoo wale wachache umemwachia nani kule nyikani? Mimi nakujua kiburi chako, na ubaya wa moyo wako; maana umeshuka ili upate kuvitazama vita.”Unaweza kuona moyo wa kaka mkubwa dhidi ya Mdogo wake akimkemea Daudi na kumuona kama kiburi na mwenye moyo mbaya! haya ndio yalikuwa aina ya maisha ya Daudi, kutokana na kuzaliwa kwake kwa utata ilihesabika kama aliyezaliwa kwa zinaa ama kwa vile Nizbeth alikuwa amekiuka makubaliano na Yese na wazee.


Kwaajili ya haya Maisha ya Daudi yalikuwa ya kudharauliwa, kukataliwa, na kuhesabika kama mtu asiyefaa kitu au aliyelaaniwa, alilaumiwa kama mtu aliyesababisha kusambaratika kwa familia, alifedheheshwa na kuonekana kama mgeni na asiyetambulika au mkimbizi, Zaburi 69:7-8 “Maana kwa ajili yako nimestahimili laumu, Fedheha imenifunika uso wangu. Nimekuwa mgeni kwa ndugu zangu, Na msikwao kwa wana wa mama yangu.” Sio tu kwa ndugu zake lakini hata jamii iliamini maneno ya ndugu wa Daudi na kufuata mfano wa familia yake Zaburi 69:10-12 “Nilipolia na kuiadhibu roho yangu kwa kufunga, Ikawa laumu juu yangu. Nilipofanya gunia kuwa nguo zangu, Nikawa mithali kwao. Waketio langoni hunisema, Na nyimbo za walevi hunidhihaki.Daudi aliishi maisha ya uchungu akimlilia Mungu kutokana na fedheha alizokutana nazo wakati wote ndugu zake walihakikisha kuwa wanampa uchungu kama chakula alifunga na kuomba na bado kwake ikawa kama ni swala la dhihaka Zaburi 69:17-21 “Wala usinifiche uso wako, mimi mtumishi wako, Maana mimi nimo taabuni, unijibu upesi. Uikaribie nafsi yangu, uikomboe, Kwa sababu ya adui zangu unifidie. Wewe umejua kulaumiwa kwangu, Na kuaibika na kufedheheka kwangu, Mbele zako Wewe wako watesi wangu wote. Laumu imenivunja moyo, Nami ninaugua sana. Nikangoja aje wa kunihurumia, wala hakuna; Na wa kunifariji, wala sikumwona mtu. Wakanipa uchungu kuwa chakula changu; Nami nilipokuwa na kiu wakaninywesha siki.Licha ya mapito ya aina hii Daudi hakuruhusiwa kuikaribia nyumba ya Bwana wala kujihusisha na maswala ya ibada, yeye na mama yake walikuwa wakisubiri siku moja kweli itadhihirika kuhusu shutuma dhidi yake na mwanaye.


Jiwe walilolikataa waashi limekuwa jiwe kuu la Pembeni!


Habari za Daudi zinabadilika sasa baada ya Nabii Samuel kuamuriwa na Mungu aende Bethelehemu kwa kusudi la kumtia mafuta moja ya watoto wa Yese ambaye yeye Mungu atamuonyesha nabii Samuel ona 1Samuel 16:1-5 “Bwana akamwambia Samweli, Hata lini utamlilia Sauli, ikiwa mimi nimemkataa asiwamiliki Israeli? Ijaze pembe yako mafuta, uende, nami nitakupeleka kwa Yese, Mbethlehemi; maana nimejipatia mfalme katika wanawe. Samweli akasema, Nawezaje kwenda? Sauli akipata habari, ataniua. Basi Bwana akasema, Chukua ndama pamoja nawe, ukaseme, Nimekuja ili kumtolea Bwana dhabihu. Ukamwite Yese aje kwenye dhabihu, nami nitakuonyesha utakayotenda; nawe utamtia mafuta yule nitakayemtaja kwako. Samweli akafanya hayo aliyosema Bwana, akaenda Bethlehemu. Wakaja wazee wa mji kumlaki, wakitetemeka, nao wakasema, Je! Umekuja kwa amani? Naye akasema, Naam, kwa amani; nimekuja kumtolea Bwana dhabihu; jitakaseni; njoni pamoja nami kwenye dhabihu. Akawatakasa Yese na wanawe, akawaita kwenye dhabihu.”



Maandiko yanaonyesha kuwa Samuel alipofika Bethelehemu wazee wa mji walikwenda kumlaki na kumsalimu na huku wakitetemeka, wote waliogopa na hofu hii haikuwa ya kawaida walihisi ujio huu wa nabii sio ujio wa kawaida hivyo walimuuliza kama amekuja kwa amani kwa mujibu wa maelezo ya marabi ni kuwa waliogopa kuwa huenda Samuel amesikia au kujulishwa dhambi yao dhidi ya kijana Daudi na labda amekuja kuwakemea vikali tabia yao na ile hali ya kumtesa kijana aliyeachwa machungani, Samuel aliwahakikishia kuwa amekuja kwa amani, na aliwataka wazee na Yese na wanae wajiunge katika ibada ya kumtolea Mungu dhabihu, Kama mzee aliyeheshimika ilikuwa ni kawaida kwa Yese kualikwa, Lakini wanae walipoalikwa hili lilikuwa jambo la kushitua kidogo, waliogopa kuwa mm huenda wamekosea sana kuwatenga watoto wa Yese na walijua kuwa labda Samuel atawakemea hadharani na kumbe Samuel alikuwa amefunuliwa kuwa Mfalme mpya ajaye ni mwana wa Yese na mbaya zaidi alikuwa ni Yule aliyekataliwa  na tena wala hakuletwa katika ibada hii ikifikiriwa kuwa hakuwa mwenye kufaa!


Swali la Samuel lilikuwa la kinabii, Mungu sio tu alimtuma kuchagua mfalme ajaye bali pia kuponya Moyo wa Nizbeth na mwanaye aliyekataliwa na jamii yake lakini pia kuuweka sawa moyo wa Yese na wazee kuwa machoni pa Mungu Yule mtoto alikuwa ni halali kwa Yese na Nezbeth na kuwa watoto wote wa Yese na Yese mwenyewe walikubaliwa na Mungu. Na wanastahili kumtumikia Mungu na kukaribia mkutano wa watu wa Mungu kama ilivyo kwa wayahudi wengine.


Swali Baada ya wana wote wa Yese kupitishwa mbele ya Samuel, Samuel alimwambia Yese Bwana hakuwachagua hawa kisha akamuuliza “Kisha Samweli akamwambia Yese, Watoto wako wote wapo hapa?  hapa ndipo palikuwa mahali pagumu sana kwa Yese kwa taarifa yako kwa vile alikuwa anaamini kuwa hawa ndio watoto wake wote angejibu tu kuwa ndio wote wapo hapa lakini ona “Naye akasema, Amesalia mdogo wao, na tazama, anawachunga kondoo” Daudi alikuwa hakubaliki na baba yake Yese alidhani kuwa mawazo ya Mungu na Samuel yatakuwa kama yake na kuwa atakubali kijana huyo abaki huko huko porini tu Lakini Samuel aliagiza aletwe mara moja na kuwa hakuna kitakachoendelea mpaka aje, kwaajili ya kumuheshimu nabii walitumwa wajumbe akamlete kijana huyo!


Inawezekana kwamba kila mmoja alishangaa tukio lile na huenda hata Samuel hakuweza kuamini kama huyu anaweza kuwa mtiwa mafuta sauti ya Mungu ikamwambia Samuel “Ondoka, umtie mafuta; maana huyu ndiye.Baada ya Samuel kumtia mafuta Sauti ya Nizbeth iliisikika ikipiga kelele za furaha kumbuka ni yeye pekee aliyekuwa akimuunga mkono mwanaye na pekee ndiye aliyekuwa faraja miaka 28 ya kuteseka kwake na ukimya wake wakikabiliwa na lawama sasa unafikia mwisho kwa Mungu kuingilia kati na kuthibitisha kuwa mtoto alikuwa na haki na mama yake alikuwa na haki na alikuwa mtoto halisi wa Yese! Na huu ukawa ndio mwisho wa mateso ya Nizbeth na mwanaye Daudi wakifurahi Nizbeth na Daudi waliimba Zaburi ya 118 na Mstari wa 22-23 wanasema maneno mazito Zaburi 118:22-23 “Jiwe walilolikataa waashi Limekuwa jiwe kuu la pembeni.Neno hili limetoka kwa Bwana, Nalo ni ajabu machoni petu.” Ilishangaza kuwa kijana aliyekataliwa na mji mzima ndiye Masihi wa bwana ndiye mpakwa mafuta ndiye mfalme ajaye! Wao walikuwa wamemkataa Daudi na Bwana alikuwa amemchagua Daudi, uchaguzi wa Daudi ulitoka kwa Mungu na ukawa ajabu kubwa sana machoni pa kila mmoja!


Kuna maswala mengi sana kuhusiana na habari hizi za siri katika maisha ya Daudi na familia yake lakini kama taarifa hizo zina ukweli na Yese na familia yake waliamini hivyo ndio maana na Daudi anayasema hayo kama taarifa ambayo ilienea katika jamii Zaburi 51:5 “Tazama, mimi naliumbwa katika hali ya uovu; Mama yangu alinichukua mimba hatiani Mstari huu umekuwa mgumu kutafasirika kwa sababu tu wayahudi hawakuwa na hawaamini katika dhambi ya asili na Daudi alipata ufunuo mdogo sana kuhusu asili ya dhambi na ndio maana tafasiri ya maandiko hayo katika mtazamo wa agano jipya ni rahisi kuliko mtazamo wa kiyahudi! hata hivyo kwa kuwa mama wa Daudi Nizbeth na mjakazi wake walikuwa na uelewa kuhusu jambo hili Daudi alifahamu pia kupitia wao kwa upande mwingine kwamba habari zile kwamba amezaliwa kwa zinaa sio za kweli, hivyo alionewa kwa sababu isiyo kweli ona  Zaburi 69:4 “Wanaonichukia bure ni wengi Kuliko nywele za kichwa changu. Watakao kunikatilia mbali wamekuwa hodari, Adui zangu kwa sababu isiyo kweli. Hata mimi nalilipishwa kwa nguvu Vitu nisivyovichukua.” na zilikuwa ni shutuma tu katika jamii yake na Mungu alilimaliza swala lile kupitia nabii Samuel na kutiwa mafuta kwa Daudi kama mwana wa Yese!.


Mapito haya ya Daudi kinabii pia yanatoa picha ya kile kilichokuwa kinaendelea katika familia ya Yusufu na Mariam, Mambo mengi yaliyompata Daudi yalikuwa ni unabii, yanatabiri jinsi mwanae yaani Masihi atakayoyapitia, Biblia haijaeleza kila kitu lakini kuna ukweli kuwa Yesu hakukubalika na Ndugu zake, Hata ingawa Mungu aliweka wazi kwa Yusufu kuwa mkewe alipata Mimba kwa uwezo wa Roho Mtakatifu, ni wazi kuwa katika jamii jambo hilo halikuweza kukubalika kama unavyoweza kufikiri Biblia inaonyesha kuwa ndugu wa Yesu Kristo walikuja kumkubali baadaye kama iliyokuwa kwa Daudi,  wao hawakumuamini kama masihi na ni Mariamu pekee ndiye aliyekuwa na uelewa kuwa Yesu ni mtoto wa namna gani kama ambavyo Nezbeth alivyomuelewa Daudi Yohana 7:1-5 “Na baada ya hayo Yesu alikuwa akitembea katika Galilaya; maana hakutaka kutembea katika Uyahudi, kwa sababu Wayahudi walikuwa wakitafuta kumwua. Na sikukuu ya Wayahudi, Sikukuu ya Vibanda, ilikuwa karibu. Basi ndugu zake wakamwambia, Ondoka hapa, uende Uyahudi, wanafunzi wako nao wapate kuzitazama kazi zako unazozifanya. Kwa maana hakuna mtu afanyaye neno kwa siri, naye mwenyewe ataka kujulikana. Ukifanya mambo haya, basi jidhihirishe kwa ulimwengu. Maana hata nduguze hawakumwamini.” Aidha watu wengine pia hawakuamini kuwa Yesu alizaliwa kwa uwezo wa Roho Mtakatifu na ili kumkatisha tamaa adui zake waliwahi kumjibu kuwa wao hawakuzaliwa kwa zinaa ona Yohana 8:41 “Ninyi mnazitenda kazi za baba yenu. Ndipo walipomwambia, Sisi hatukuzaliwa kwa zinaa; sisi tunaye Baba mmoja, yaani, Mungu.” Unaweza kuona kwa ufupi mapito aliyopitia Daudi kinabii yalimtokea Yesu Kristo! Daudi anaposema mama yangu alinichukua Mimba hatiani wakati huu hakukuwa na ufunuo wa mwanadamu kuwa na asili ya dhambi, kwa hivyo watafasiri wengi wa biblia wakiwemo marabi, walikuwa wanafikri kuwa Daudi alikuwa akiizungumzia hali ya maneno yaliyoenea katika jamii yaje kuwa mama yake alimchukua mimba hatiani, na kama yalikuwa ni mapatano na Yese kuwa wasikutane ni dhahiri kuwa Nizbeth alifanya makosa kuchukua mimba na Yese nje ya mapatano na amri ya wazee, lakini kama mke halali wa Yese mama huyu ni shujaa wa imani kwani kupitia tendo hili, alivishinda vita vya kishetani vya kupamaba na uzao wa Masihi.


Sasa basi Daudi alikuwa na maana gani kusema mama yangu alinichukua Mimba hatiani kama tunaona kuwa Daudi ni mwana halali wa Yese hapa kuna mawazo mbalimbali kuhusu tafasiri za mstari huu ukiacha masimulizi ya Kiyahudi:-


2.       Asili ya dhambi: Mstari huu pia unaweza kumaanisha kuwa watoto wachanga wanazaliwa wakiwa na dhambi ya asili, kwamba tendo la Daudi kufanya dhambi, licha ya kuwa ni mtu aliyeupendeza moyo wa Mungu na bado alikuwa analenga kumpendeza Mungu na kamwe hakwepi ule wajibu wa kuwa anawajibika kwa Mungu kwa dhambi aliyoitenda lakini anapata utambuzi kuwa ameumbwa katika hali hiyo na sio kwaajili ya Muumba mwenyewe lakini kwa kurithi, kwa damu, tangu alipokuwa akitungishwa mimba au tangu mama yake anapokea ujauzito kuhusu yeye tayari alikuwa na dhambi ya asili inayotokana na uwepo wa dhambi kwa baba yetu Adamu Ezekiel 16:4 . “Na katika habari za kuzaliwa kwako, siku ile uliyozaliwa, kitovu chako hakikukatwa, wala hukuoshwa kwa maji usafishwe; hukutiwa chumvi hata kidogo, wala hukutiwa katika nguo kabisa.Ezekiel anazungumzia kitovu cha kiroho japo kila mtoto anapozaliwa anakatwa kitovu, lakini kuna kitovu cha rohoni kinachotuunga kurithi maswala kadhaa kutoka kwa baba zetu kwa hiyo sisi tumefanya dhambi tangu tukiwa viunoni mwa baba yetu Adamu kama vile maandiko yanavyotufundisha kuwa Lawi alitoa zaka wakati Abraham anatoa zaka kwa Melkizedeki kwa vile alikuwa katika viuno vyake ona Waebrania 7:9-10 “Tena yaweza kusemwa ya kuwa, kwa njia ya Ibrahimu, hata Lawi apokeaye sehemu ya kumi alitoa sehemu ya kumi; kwa maana alikuwa katika viuno vya baba yake, hapo Melkizedeki alipokutana naye.Kwa hivyo watoto wanarithi hatia kutoka kwa wazazi wao, na wanashiriki mema kutoka kwa wazazi wao kitendo cha Abrahamu kutoa zaka kinahesabika kibiblia kuwa Lawi naye alitoa zaka hata kabla ya kuzaliwa kwa vile alikuwa viunoni mwa baba yake na ndio maana watoto vilevile hufa kwa sababu mshahara wa dhambi ni mauti ona Warumi 6:23 “Kwa maana mshahara wa dhambi ni mauti; bali karama ya Mungu ni uzima wa milele katika Kristo Yesu Bwana wetu.” Urithi wa kifo umetokana na urithi wa dhambi  na vyote hivi tumevirithi kutoka kwa Adamu baba yetu kwa msingi huo wanadamu wote ni wenye dhambi isipokuwa Yesu Kristo pekee, sasa basi Daudi anapotubia kosa lake anaakisi asili yake ya dhambi kwa kusema Tazama mimi naliumbwa katika hali ya uovu, mama yangu alinichukua mimba hatiani, akimaanisha kuwa alikuwa mwenye dhambi tangu inatungishwa mimba, kama vile adui alivyopanda magugu kwenye ngano mapema kabla havijaanza kuota na hii ilikuwa moja ya dhana ya kiyahudi pia kwamba mwanadamu huzaliwa katika hali ya dhambi Yohana 9:34 “Wakajibu, wakamwambia, Ama! Wewe ulizaliwa katika dhambi tupu, nawe unatufundisha sisi? Wakamtoa nje.” Hii inaweza kuwa tafasiri nzuri ya andiko hilo kwa mtazamo wa kikristo, japo katika agano la kale mtazamo huu na kwa wayahudi ulikuwa haujafunuliwa wazi.


3.        Mwenye dhambi kwa kuzaliwa: Daudi hapa ni kama anatambua kuwa yeye sio mwenye dhambi tu kwa kuzitenda lakini pia ni mwenye dhambi kwa kuzaliwa au kwa asili, Paulo mtume aliliambia kanisa la warumi kwamba Warumi 5:12 “Lakini karama ile haikuwa kama lile kosa; kwa maana ikiwa kwa kukosa kwake yule mmoja wengi walikufa, zaidi sana neema ya Mungu, na kipawa kilicho katika neema yake mwanadamu mmoja Yesu Kristo kimezidi kwa ajili ya wale wengi.” Wala Daudi hakumaanisha kuwa tendo la ndoa katika ndoa ni dhambi, au mimba iliyotungwa kwa wazazi wake halali ilikuwa kosa lakini alikuwa na wazo kuwa mwanadamu ana asili ya uharibifu tu, Kama jinsi ambavyo mwembe huzaa mwembe, Mwanadamu hufanya dhambi kwa sababu ni mwenye dhambi kwa asili Warumi 3:10-12, 23 ”kama ilivyoandikwa, ya kwamba, Hakuna mwenye haki hata mmoja. Hakuna afahamuye; Hakuna amtafutaye Mungu. Wote wamepotoka, wameoza wote pia; Hakuna mtenda mema, la! Hata mmoja., kwa sababu wote wamefanya dhambi, na kupungukiwa na utukufu wa Mungu;Kwa msingi huo kwa vile wanadamu wote ni wenye dhambi kwa asili na kwa kuzitenda, hatuwezi kuingia katika ufalme wa Mungu bila kupokea asili mpya kwa neema ya Yesu Kristo na ndio maana pamoja na dua yake Daudi alijiombea moyo safi na kuumbwa upya kwa roho yake ona Zaburi 51:10-11 ”Ee Mungu, uniumbie moyo safi, Uifanye upya roho iliyotulia ndani yangu Usinitenge na uso wako, Wala roho yako mtakatifu usiniondolee.” Wakati huu kazi za Kristo na Roho Mtakatifu zilikuwa sio dhahiri sana Lakini Daudi alikuwa na hisia za kinabii za kutamani kuzaliwa mara ya pili ili asili yake ya dhambi iweze kudhoofishwa kwa msaada wa Roho Mtakatifu na kufanywa upya Yohana 3; 4-7 “Nikodemo akamwambia, Awezaje mtu kuzaliwa, akiwa mzee? Aweza kuingia tumboni mwa mamaye mara ya pili akazaliwa? Yesu akajibu, Amin, amin, nakuambia, Mtu asipozaliwa kwa maji na kwa Roho, hawezi kuuingia ufalme wa Mungu. Kilichozaliwa kwa mwili ni mwili; na kilichozaliwa kwa Roho ni roho. Usistaajabu kwa kuwa nilikuambia, Hamna budi kuzaliwa mara ya pili.Mungu anapoingilia kati na kudhoofisha asili ya dhambi ndipo tunapata neema ya kuwa washirika wa tabia ya uungu ndani yetu 2Petro 1:4 “Tena kwa hayo ametukirimia ahadi kubwa mno, za thamani, ili kwamba kwa hizo mpate kuwa washirika wa tabia ya Uungu, mkiokolewa na uharibifu uliomo duniani kwa sababu ya tamaa.” Bila neema ya Mungu na uwezo war oho Mtakatifu kuingilia kati na kudhoofisha nguvu ya asili ndani yetu hatuwezi kuchagua kutokuitenda dhambi, isipokuwa kwa msada wa Mungu.


4.       Dhana ya tangu ujana au utoto: Daudi alikuwa kwenye maombi binafsi na toba yake kwa Mungu alikuwa ameelewa kuwa amemkosea Mungu na wala hakuwa anatafuta kujitetea kwa Mungu wake wala kusingizia dhambi yake kwa wazazi wake wala kujihesabia haki, Ezekiel 18:20 “Roho itendayo dhambi, ndiyo itakayokufa; mwana hatauchukua uovu wa baba yake, wala baba hatauchukua uovu wa mwanawe, haki yake mwenye haki itakuwa juu yake, na uovu wake mwenye uovu utakuwa juu yake.” Daudi alikuwa anataka kuikamilisha toba yake kwamba sio tu nimekutenda dhambi binafsi, lakini kwa asili mimi ni mwenye dhambi, Matendo ya maisha yangu yameathiriwa tangu namna ya kuumbwa kwangu na hata kuzaliwa kwangu, Mama yangu alinichukua mimba hatiani, hamaaniishi anataka kumshutumu mama yake yeye alikuwa akijianika kwa Mungu na kumueleza Mungu mtazamo wake kwamba anastahili kuwa chombo cha hasira ya Mungu,  lakini zaidi sana anahitaji rehema, zaidi ya dhambi aliyoifanya lakini hata na tangu kuzaliwa kwake na kuumbika kwake ndani ya tumbo la mama yake. Mzizi wake wa dhambi unatoka mbali. Daudi anakubali kuwajibika kwa dhambi yake wala hamtwishi awaye yote maovu yake, kuumbwa katika hali ya uovu kwake pia haimaanishi kuwa anamlaumu Mungu muumba bali yeye anakubali kuwa mwanadamu kwaasili ni muovu, wayahudi wakati mwingine walitumia neno ujana, wakimaanisha vievile hatua za ukuaji kutoka mwaka 0-28 miaka ya ujana kwa hiyo walikuwa na semi kama mwanadamu ameharibika tangu ujana wake wakiwa na maana tangu mtu anajua mema na mabaya ona kwa mfano au tangu anaanza maisha Mwanzo 8:21 “BWANA akasikia harufu ya kumridhisha; BWANA akasema moyoni, Sitailaani nchi tena baada ya hayo kwa sababu ya wanadamu, maana mawazo ya moyo wa mwanadamu ni mabaya tangu UJANA wake; wala sitapiga tena baada ya hayo kila kilicho hai kama nilivyofanya.” Ona pia Yeremia 3:25 “Na tulale kwa aibu yetu, haya yetu na itufunike; kwa maana tumemwasi Bwana, Mungu wetu, sisi na baba zetu, tangu UJANA wetu hata leo; wala hatukuitii sauti ya Bwana, Mungu wetu.” Isaya 7:15 “Siagi na asali atakula, wakati ajuapo kuyakataa mabaya na kuyachagua mema.” Waebrania walikuwa na dhana kuwa mwanadamu huanza kuhesabiwa haki wakati wa ujana wake yaani wakati ajuapo kutenda mema au mabaya Lakini Daudi anaona kuwa tangu mimba inapotungwa tayari hali ya kutenda tusiyoyataka inampata mwanadamu.

5.       Lugha ya kimashairi


Wengine hudhani kuwa Zaburi 51:5 ni Lugha ya kishairi tu ya kukuza mambo “hyperbole” Daudi alikuwa anatubu dhambi na kuikiri dhambi aliyokuwa ameifanya mbele za Mungu na kati kati ya toba yake  anajutia na kujikuza kuwa yeye ni mwenye dhambi zaidi ya kawaida na kuwa amekuwa mwenye dhambi kwa asili tangu kutungishwa mimba, Kwa hiyo wataalamu wa kimaandiko hufikiri kuwa ni lugha tu ya kishairi kama vile mtu anavyoweza kusema analowesha kitanda chake kwa machozi Zaburi 6:6 “Nimechoka kwa kuugua kwangu; Kila usiku nakieleza kitanda changu; Nalilowesha godoro langu kwa machozi yangu au kama vile Paulo anavyodai kuwa Mungu alikuja kuwaokoa wenye dhambi na wa kwanza wao ni mimi 1Timotheo 1:15  Ni neno la kuaminiwa, tena lastahili kukubalika kabisa, ya kwamba Kristo Yesu alikuja ulimwenguni awaokoe wenye dhambi; ambao wa kwanza wao ni mimi.”   

         
6.       Lugha tu!


Wakati mwingine Lugha tu inaweza kusababisha mstari uweze kuwa mgumu kutafasirika kwa msingi huo tunapoangalia lugha zilizotumika katika Biblia mbalimbalia utaweza kugundua kuwa lugha iliyotumika hapo imefanywa kuwa ngumu na baadhi ya tafasiri za biblia na baadhi zimeifanya kuwa rahisi kwa Mfano:-

NIV Psalm 51:5 “Surely I was sinful at Birth, sinful from time my mother conceived me “Kwa hakika nalikuwa mwenye dhambi tangu kuzaliwa, mwenye dhambi tangu mama yangu anatunga ujauzito”

KJV Psalm 51:5 “Behold I was shapen in iniquity, and in sin did my mother conceive me” Tazama nimeumbwa katika hali ya uovu, na katika hali ya dhambi mama yangu alinipokea”

ESV.Psalm 51:5 “Behold I was brought forth in iniquity, and in sin did my mother conceive me” Tazama naliletwa katika hali ya uovu na katika hali ya dhambi mama yangu alinipokea

NLT Psalm 51:5 “For I was born a sinner,Yes from the moment my mother conceived me” Kwa dhambi nalizaliwa ndio tangu wakati mama yangu ananipokea”

SUV Zaburi 51:5 ““Tazama, mimi naliumbwa katika hali ya uovu; Mama yangu alinichukua mimba hatiani

Tunajifunza kwamba wakati mwingine ili andiko liweze kuekleweka vema tunaweza kupitia tafasiri mbalimbali za kimaandiko na tukapata maana iliyokusudiwa kwa njia rahisi, na kifungu au mstari ukawa ni mwepesi kueleweka.


7.       Tamaa ya mama

Kwa mujibu wa uchunguzi wa ndani zaidi wa kimaandiko wenye lengo la kuuangalia mstari huu bila kuwa na mtazamo wa Kikrito wa kuwa mwanadamu ni mwenye dhambi kwa asili, unapoangalia Lugha zilizotumika hapa ni wazi kuwa Daudi hamaanishi dhambi kutoka kwa Adamu, bali anamaanisha dhambi ya mama yake, yaani kuwa mama yangu alinichukua mimba hatiani, bila kuweka mtazamo wa Kikristo unapochunguza maneno yaliyotumiwa na Daudi katika Mstari huu kuhusu mama yake kumchukua mimba hatiani kwa kawaida kwa waebrania neno kushika mimba au kuchukua mimba linatumika neno “HARAH” ambalo linamaanisha kuwa mwanamke ameshika mimba, sasa katika kifungu hiki Daudi anatumia neno “YACHAN” ambalo neno hili ni baya sana kutumika kwa mwanadamu neno hili linamaanisha kushika mimba katika tama ya kinyama yaani kama vile kondoo au Mbuzi ama Ngombe anavyopandisha joto akiwa anataka kupata ujauzito ndio hali inayoitumia Daudi kwa mama yake kuwa mjamzito, kwa hiyo huenda Daudi anamaanisha ile tama ya mama yake ya kutaka kupokea ujauzito ilikuwa ni tama kama ya mnyama mwenye joto, kwa hiyo Daudi anapotumia neno YACHAN anatumia neno gumu sana kuonyesha kwamba alizaliwa akiwa na hali ya tama na mama yake alimchukua mimba katika hali ya tama ambayo ni tama kama ile ya mnyama kwa hiyo mimba ya daudi ilipatikana kama matokeo ya tama ya mama yake iliyokuwa kama ya mnyama na huenda kwa tamaa kama ile ya Nizbeth naye alifanya unyama kumkabili mke wa Uria, Hivyo basi kama Nizbeth hakufanya zinaa kumpata Daudi, alimpata kwa kuvunja patano alilowekewa, alimpata kama matokeo ya tama kali ya mama yake Zaburi 51:5 ““Tazama, mimi naliumbwa katika hali ya uovu; Mama yangu alinichukua mimba hatianihuu unaweza kuwa Mtazamo sahihi wa andiko hili kama hatutaweka fundisho la mwanadamu kuzaliwa akiwa na asili ya dhambi, lakini bado tunaona urithi wa aina ileile ya asili ya dhambi kwamba kama kulikuwa na tamaa ya kinyama kwa Nizbeth, Mwanae naye aliipata kwa Nizbeth na kama hivyo ndiyo ni tama ileile ya Eva kutamani lile tunda katika bustani ya edeni 


Hitimisho!


Ni muhimu kukubali kuwa Mstari huu ni mstari wa Msingi sana na dhana zote zinazotolewa na wanatheolojia kuhusu Mstari huu ni za msingi sana, zote zinatusaidia kufikiri vema na kujifunza vema neno la Mungu, Nimefurahia mtazamo wa kiyahudi kuhusu mstari huu kwa sababu ziko kweli kadhaa kuwa kuna mambo tulikuwa hatuyafahamu kuhusu maisha ya Daudi, sasa tunaweza kuisoma zaburi katika mtazamo mpana mno na kuelewa maumivu aliyoyapitia kijana huyu, lakini vilevile kinabii tunapata picha ya wazi kuhusu kile alichokipitia Mariamu na Mwanaye Yesu Kristo, kwamba kinafanana kwa ukaribu na kile kilichompata Daudi na Nizbeth!


Lakini ninaporejea sasa katikamstari wa msingi wa Zaburi 51:5 Tazama, mimi naliumbwa katika hali ya uovu; Mama yangu alinichukua mimba hatianinaweza kuhitimisha kwa kusema haya Daudi hamaanishi kuwa Tendo la ndoa katika ndoa halali ni dhambi, wala hamaanishi kwamba kutungishwa mimba kwa mama yake na baba yake ni dhambi, Daudi aliwaheshimu sana Wazazi wake na kuwatunza na amani iliporeja nyumbani kwao ni yeye ndiye aliyewapeleka na kuwatunza kwa mfalme wa Moabu ona 1Samuel 22:3-4. “Kutoka huko Daudi akaenda Mispa ya Moabu; akamwambia mfalme wa Moabu, Tafadhali ukubali BABA YANGU NA MAMA YANGU watoke huko waliko, wakakae kwenu, hata nitakapojua Mungu atakalotenda kwa ajili yangu. Akawaleta mbele ya mfalme wa Moabu, nao wakakaa pamoja naye wakati wote Daudi alipokuwa ngomeni.” Ni wazi kuwa kama kulikuwa na utata uliisha baada ya Samuel Nabii kumaliza tatizo, Kwa hiyo ni dhahiri Mungu alitambua kuwa Yese na Nezbeth walikuwa wazazi halali wa Daudi na mapito yalikuwa ya kinabii tu, Daudi aliwaheshimu baba yake na mama yake na aliwatunza na kuhakikisha wako salama, Daudi hamaanishi kuwa alizaliwa kwa zinaa, kama mama yake alikwenda kwa mumewe usiku na kupata ujauzito bado ilikuwa ni ndoa halali, na iliathiriwa tu na utafutaji wa kweli za uchambuzi wa torati, tendo la Ndoa ni takatifu na ni zawadi ya Mungu na Mungu ameamuru kuwa ndoa na ziheshimiwe Waebrania 13:4, Zaburi 51:5 ni wazi kabisa kuwa kwa mtazamo na ufunuo wa kiagano jipya unamaanisha kuwa kwa kuwa sisi ni watoto wa Adamu tunazaliwa na hali Fulani ndani yetu inayotusukuma kuasi hata wakati mwingine mioyo yetu ikiwa haipendi, kwa hiyo kwa bidii ya kibinadamu hatuwezi kamwe kuishinda dhambi bila msaada wa kiungu Warumi 7:21-24 “Basi nimeona sheria hii, ya kuwa kwangu mimi nitakaye kutenda lililo jema, lipo lililo baya. Kwa maana naifurahia sheria ya Mungu kwa utu wa ndani, lakini katika viungo vyangu naona sheria iliyo mbali, inapiga vita na ile sheria ya akili zangu, na kunifanya mateka ya ile sheria ya dhambi iliyo katika viungo vyangu.Ole wangu, maskini mimi! Ni nani atakayeniokoa na mwili huu wa mauti?  Namshukuru Mungu, kwa Yesu Kristo Bwana wetu. Basi, kama ni hivyo, mimi mwenyewe kwa akili zangu naitumikia sheria ya Mungu, bali kwa mwili wangu sheria ya dhambi.” Kwa ufunuo Fulani Daudi aliishia kusema aliumbwa katika hali ya uovu na alichukuliwa mimba hatiani, lakini ni wazi alikuwa ni kama mtu anayejiuliza ilikuwaje hata akatenda uovu ule mkubwa mtu ambaye moyo wake siku zote ulikuwa unalenga kumpendeza Mungu, kwa hiyo Daudi ni kama alitaka kusema hili anachokisema Paulo Mtume kuwa iko sheria ndani yetu ambayo inapingana na lile jema unalotaka kulitenda  na ni kwa msaada wa Roho Mtakatifu tu na Kazi aliyoifanya Yesu msalabani tutaweza kuwa huru kutoka katika vita vyetu vya asili vinavyotupinga ndani kwa ndani kama nguvu ya “gravitation force” ama nia ya mwili Warumi 7:24-25 “Ole wangu, maskini mimi! Ni nani atakayeniokoa na mwili huu wa mauti? Namshukuru Mungu, kwa Yesu Kristo Bwana wetu. Basi, kama ni hivyo, mimi mwenyewe kwa akili zangu naitumikia sheria ya Mungu, bali kwa mwili wangu sheria ya dhambi.” Na Warumi 8:1-3 “Sasa, basi, hakuna hukumu ya adhabu juu yao walio katika Kristo Yesu. Kwa sababu sheria ya Roho wa uzima ule ulio katika Kristo Yesu imeniacha huru, mbali na sheria ya dhambi na mauti. Maana yale yasiyowezekana kwa sheria, kwa vile ilivyokuwa dhaifu kwa sababu ya mwili, Mungu, kwa kumtuma Mwanawe mwenyewe katika mfano wa mwili ulio wa dhambi, na kwa sababu ya dhambi, aliihukumu dhambi katika mwili;
               
Na Rev. Innocent Kamote
Mkuu wa wajenzi mwenye hekima
0718990796