Jumamosi, 3 Agosti 2019

Jicho kwa jicho na jino kwa jino!


Mathayo 5:38-41Mmesikia kwamba imenenwa, Jicho kwa jicho, na jino kwa jino; Lakini mimi nawaambia, Msishindane na mtu mwovu; lakini mtu akupigaye shavu la kuume, mgeuzie na la pili. Na mtu atakaye kukushitaki na kuitwaa kanzu yako, mwachie na joho pia. Na mtu atakayekulazimisha mwendo wa maili moja, nenda naye mbili.






Utangulizi:
Ni muhimu kufahamu kuwa usemi huu Jicho kwa jicho  na jino kwa jino una asili yake kutoka katika sheria  za ukaldayo zilizojulikana kama sheria za “Hammurabi”, lakini vilevile zinapatikana katika sheria ya Musa yaani agano la kale hususani katika kitabu cha Kutoka na kile kitabu cha Walawi, Zaidi ya yote Yesu aligusia juu ya hili katika hutuba yake ya mlimani katika agano jipya, Maana yake katika maandiko ikiwa ni rahisi tu “kuwa atendaye uovu anastahili kupata adhabu sawa sawa na kosa lake”
Ni muhimu kufahamu kuwa sheria ya Musa ilipotolewa ilikuwa imezingatia maeneo makubwa matatu yakiwemo ya Kidini, Kimaadili na kisiasa au kisheria yaani ninaweza kukuchanganulia sheria au Torati katika mazingira matatu yafuatayo:-
1.       Ceremonial law – Sheria za maswala ya kidini namna na jinsi impaswavyo mtu kumuabudu Mungu.
2.       Moral law – Sheria za uadilifu maswala ya mahusiano na kuishi kwa amani na watu wote.
3.       Civil law – Sheria za kimahakama na kifalme namana na jinsi serikali inavyoweza kuendeshwa.
Kwa msingi huo sheria au usemi huu wa Jicho kwa jicho na jino kwa jino, unaangulkia katika maswala ya kimahakama ambayo kimsingi yanaangukia katika swala la sheria za kiutawala Civil Law, mbele ya hakimu/jaji au mwamuzi kwa msingi huo usemi wa jicho kwa jicho na jino kwa jino  ni usemi wenye kuonyesha msisitizo au kuonya Mahakimu na majaji au waamuzi kuhukumu kwa haki, kutenda haki, wanapoamua kesi za watu na Yesu hakuwa na neno juu ya hili.

Wajibu wa Mahakama na sheria  zetu leo Duniani.
Ni muhimu kufahamu kuwa sheria hii ya kimahakama Yesu hakuiondoa Mathayo 5:17Msidhani ya kuwa nalikuja kuitangua torati au manabii la, sikuja kutangua, bali kutimiliza” Yesu anataka mahakama na sheria zetu duniani kuzingatia usawa katika kutoa haki, Kama ilivyoagizwa katika torati, na  yeye analikabidhi jukumu hili kwa mamlaka za  kila taifa na serikali na ufalme, hususani mahakama zake kwamba zinapaswa kuwapa watu haki zao, zina wajibu wa kutimiliza majukumu yao kwa mujibu wa sheria, lakini vilevile Mabunge kuhakikisha kuwa yanapitia sheria zote zilizopitwa na wakati na zisizotoa haki kwa upande mmoja, kuhakikisha kuwa haki inatendeka, huku kila mtu akistahili malipo kulinga na kile alichokifanya, haki inaposimama inastawisha taifa zima, Mithali 14:34Haki huinua Taifa ; Bali dhambi ni aibu ya watu wote” Ustawi wa jamii nzima unakuja pale tu haki inapotendeka, Mungu anataka haki itendeke, kadiri Dunia inavyoharibika ndivyo jinsi haki inavyozidi kuwa bidhaa adimu, Taifa lolote, familia yoyote na taasisi yoyote na ufalme wowote ambao hautendi haki, utaangushwa lakini Mungu hustawisha na kuinua taifa ambalo linatenda haki, kwa msingi huo kila jamii ina wajibu wa kujenga tabia na mwenendo wa kutenda haki, ili tuweze kubarikiwa na Mungu, Mungu hawezi kutubariki wakati tukiwa tumejaa udhalimu au taifa lililojaa dhuluma.Aidha watu hukosa amani na furaha wanapotawaliwa na watu waovu au watu wasiosimamia haki na usawa Mithali 29:2Wenye haki wakiwa na amri watu hufurahi, Bali mwovu atawalapo watu huugua” Furaha na amani ya kweli katika jamii inapatikana kwa utawala wa haki, wenye kuhukumu kwa haki na kumuacha muovu awajibike kwa kile alichokifanya, Huu ndio mpango wa Mungu.

Kwa msingi huu Kanuni ya kutenda haki kwa mujibu wa Yesu kwa upande wa utawala inabaki vile vile katika kuhakikisha mahakama, wanasheria na Majaji na waamuzi wanatenda haki, wakiongozwa na kanuni, na sheria za jamii husika, huku sheria hii kutoka katika torati ya Musa ikiwa ndio msingi wa swala hili, wao wana wajibu wa kuwapatia watu haki zao, na kila jamii inapaswa kufanya hivyo hii ndio maana ya usemi wa Jicho kwa jicho na jino kwa jino.

Wajibu wa wanafunzi wa Yesu!
Baada ya Yesu kukamilisha fundisho juu ya umuhimu wa haki, ni muhimu kufahamu kuwa Yesu hakuondoa umuhimu wa kudai haki inayostahili, haki inapaswa kusimama vilevile kama ipaswavyo, watendao maovu wanapaswa kulipia uovu wao,lakini hili ni jukumu la kiutawala

Warumi 13:1-5 “Kila mtu na aitii mamlaka iliyo kuu; kwa maana hakuna mamlaka isiyotoka kwa Mungu; na ile iliyopo umeamriwa na Mungu. Hivyo amwasiye mwenye mamlaka hushindana na agizo la Mungu; nao washindanao watajipatia hukumu. Kwa maana watawalao hawatishi watu kwa sababu ya matendo mema, bali kwa sababu ya matendo mabaya. Basi, wataka usimwogope mwenye mamlaka? Fanya mema, nawe utapata sifa kwake; kwa kuwa yeye ni mtumishi wa Mungu kwako kwa ajili ya mema. Lakini ufanyapo mabaya, ogopa; kwa maana hauchukui upanga bure; kwa kuwa ni mtumishi wa Mungu, amlipizaye kisasi mtenda mabaya kwa ajili ya ghadhabu. Kwa hiyo ni lazima kutii, si kwa sababu ya ile ghadhabu tu, ila na kwa sababu ya dhamiri.
Kwa kuwa serikali zipo basi kila atendaye uovu anapaswa kulipwa sawa na haki za kisheria zilizoko katika utawala husika, Lakini wanafunzi wa Yesu kwa mujibu wa Mafundisho yake wanapaswa kuwa na uadilifu na kwenda mbali zaidi kuliko sheria inavyotaka ili mwenendo wao uweze kuwahubiri waovu wajue kuwa yuko Mungu, kwa hivyo kwa kupitia upendo wana wanapaswa kuwapenda adui zao, kuwa na utayari hata wa kuwasamehe  na kupoteza haki zao za kisheria na kuwalipa mema badala ya mabaya, Yesu anawataka wanafunzi wake kutokuitikia jambo lolote ovu katika namna ya chuki au kulipa baya kwa baya Mungu anataka tuushinde ubaya kwa wema

Warumi 12:17-21.Msimlipe mtu ovu kwa ovu. Angalieni yaliyo mema machoni pa watu wote. Kama yamkini, kwa upande wenu, mkae katika amani na watu wote. Wapenzi, msijilipize kisasi, bali ipisheni ghadhabu ya Mungu; maana imeandikwa, Kisasi ni juu yangu mimi; mimi nitalipa, anena Bwana. Lakini, Adui yako akiwa na njaa, mlishe; akiwa na kiu, mnyweshe; maana ufanyapo hivyo, utampalia makaa ya moto kichwani pake. Usishindwe na ubaya, bali uushinde ubaya kwa wema.”,

Yesu katika mafundisho yake anataka Wakristo tuonyeshe muitikio wenye uadilifu unaoonyesha kuwa sisi ni wanafunzi wa Yesu ili kupitia wema wetu walio gizani waweze kuiona Nuru, jambo hili ndilo linaloleta thawabu kwa Mungu, yaani watu wanapotukusudia mabaya sisi tuwakusudie mema tu

Mwanzo 50:19-21 “Yusufu akawaambia, Msiogope, je! Mimi ni badala ya Mungu? Nanyi kweli mlinikusudia mabaya, bali Mungu aliyakusudia kuwa mema, ili itokee kuokoa taifa kubwa, kama ilivyo leo. Basi sasa msiogope; mimi nitawalisha na watoto wenu. Akawafariji, na kusema nao vema.”
Yusufu alichukiwa bure tu na ndugu zake na tena walikusudia kumuua 

Mwanzo 37:18 “ Wakamwona  toka mbali na kabla hajawakaribia, wakafanya shauri juu yake ili wamuue”
kabisa na baadaye waliamua kumuuza utumwani, angeweza Yusufu kujilipizia kisasi lakini alionyesha mwitikio mwema alisema nao vizuri na aliwalisha wana na watoto zao ili Nduguze waweze kuuona wema wa Mungu katika uovu wao, Hiki ndicho Yesu alichokuwa amekikusudia katika neno lake, Yesu anawataka wakristo wavumilie na hatimaye wamuachie Mungu awalipizie Kisasi dhidi ya wale wote wanaotaka kuangamiza maisha yetu Bwana ataamua yeye mwenyewe lakini mkono wako usiwe juu ya adui yako anayekutafuta na Mungu atafanya tu 1Samuel 24:1-22, “Ikawa, Sauli aliporudi baada ya kuwafuatia Wafilisti, aliambiwa ya kwamba, Daudi yuko katika nyika ya Engedi. Ndipo Sauli akatwaa watu elfu waliochaguliwa katika Israeli wote, akaenda kumtafuta Daudi na watu wake juu ya majabali ya mbuzi-mwitu. Akafika penye mazizi ya kondoo kando ya njia, na huko kulikuwa na pango; Sauli akaingia ndani ili kuifunika miguu. Na Daudi na watu wake walikuwa wakikaa mle pangoni ndani sana. Nao watu wa Daudi wakamwambia, Tazama, hii ndiyo siku ile aliyokuambia Bwana, Angalia, nitamtia adui yako mikononi mwako, nawe utamtenda yo yote utakayoona kuwa mema. Basi Daudi akainuka, akaukata upindo wa vazi lake Sauli kwa siri. Lakini halafu, moyo wake Daudi ukamchoma, kwa sababu amekata upindo wa vazi lake Sauli. Akawaambia watu wake, Hasha! Nisimtendee bwana wangu, masihi wa BWANA,neon hili,kuunyosha mkono wangu juu yake,kwa maana yeye ni masihi wa BWANA. Basi Daudi akawazuia watu wake kwa maneno hayo, asiwaache kumwondokea Sauli. Kisha Sauli akatoka pangoni, akaenda zake. Daudi naye akainuka baadaye, akatoka pangoni, akamwita Sauli, akisema, Bwana wangu, mfalme. Na Sauli alipotazama nyuma, Daudi akainama uso wake hata nchi, akamsujudia. Daudi akamwambia Sauli, Kwa nini unasikiliza maneno ya watu wasemao, Tazama, Daudi anataka kukudhuru? Tazama, leo hivi macho yako yameona jinsi Bwana alivyokutia mikononi mwangu pangoni, na watu wengine wakaniambia nikuue; lakini nikakuacha; nikasema, Sitaki kuunyosha mkono wangu juu ya bwana wangu; kwa maana yeye ni masihi wa BWANA.Tena, baba yangu, tazama, tafadhali, tazama upindo wa vazi lako mkononi mwangu; maana ikiwa nimeukata upindo wa vazi lako, nisikuue, ujue, na kuona ya kuwa hakuna uovu wala kosa mkononi mwangu, wala sikukukosa neno; ingawa wewe unaniwinda roho yangu ili kuikamata. Bwana atuamue, mimi na wewe, na Bwana anilipizie kisasi changu kwako; lakini mkono wangu hautakuwa juu yako. Kama vile walivyosema watu wa kale katika mithali yao, Katika waovu hutoka uovu; ila mkono wangu hautakuwa juu yako. Na mfalme wa Israeli ametoka ili kumfuatia nani? Unamwinda nani? Ni kuwinda mbwa mfu, au kiroboto. Basi Bwana atuamue, akatuhukumu mimi na wewe, akaone, akanitetee neno langu, akaniokoe na mkono wako. Ikawa, Daudi alipokwisha kumwambia Sauli maneno hayo Sauli alisema, Hii ndiyo sauti yako, Daudi, mwanangu? Naye Sauli akapaza sauti yake, akalia.  Akamwambia Daudi, Wewe u mwenye haki kuliko mimi; maana wewe umenitendea mema, nami nimekutenda mabaya. Nawe umeonyesha leo jinsi ulivyonitendea mema, kwani Bwana aliponitia mikononi mwako, hukuniua.Maana mtu akimwona adui yake, je! Atamwacha aende zake salama? Basi Bwana na akulipe mema kwa haya uliyonitendea leo.  Na sasa, angalia, najua ya kuwa hakika utakuwa mfalme, na ufalme wa Israeli utafanyika imara mkononi mwako. Basi sasa, uniapie kwa Bwana, ya kwamba hutawakatilia mbali wazao wangu baada yangu, wala hutaliharibu jina langu katika mbari ya baba yangu. Naye Daudi akamwapia Sauli. Kisha Sauli akaenda zake kwao; lakini Daudi na watu wake wakapanda kwenda ngomeni.”
Unaweza kuona kwa msingi wa mafundisho hayo Yesu alikuwa anataka tuachilie haki zetu kwa kuutanguliza upendo hata kwa wale ambao ni adui zetu na sio hivyo tu hata kuwaombea, hii haina maana kuwa Mungu hataingilia kati hapana Mungu atawalipa wale wanaotutendea uovu watavuna kila walichokipanda kama hawatatubu na kubadilika kupitia wema wetu, kwa kuwa  Mungu hadhiahakiwi, Yesu alitaka tusishindane na mtu muovu, tusikae katika kanuni ya jicho kwa jicho au jino kwa jino alitaka tuonyeshe upendo wa Mungu kwa adui zetu ili waweze kujutia maovu yao kama ilivyotokea kwa Sauli na ndugu za Yusufu. Walitenda dhambi walikusudia mabaya Lakini Daudi na Yusufu walikusudia mema.

Warumi 12:20 “Lakini adui yako akiwa na njaa mlishe na akiwa na kiu mnyweshe, maana ufanyapo hivyo utampalia makaa ya moto kichwani
Mungu kwa neema yake na kwa wakati wake atalipa kisasi, kisasi ni juu yake Lakini sio hivyo tu tunaporejesha mema kwa waliotutenda uovu meama yatakaa katika nyumba zetu yaani ukoo wetu wote utabarikiwa lakini tukirejesha mabaya badala ya mema mabaya hayataondoka katika nyumba yetu yaani ukoo wetu

Mithali 17:13 “Yeye arudishaye mabaya badala ya mema, Mabaya hayataondoka nyumbani mwake.”
Kwa msingi huo kuba baraka kubwa sana mbele za Mungu na Mbele za Bwana wetu Yesu Kristo katika kulitendea kazi lile alilotuagiza  Yohana 13:17 “Mkiyajua hayo, heri ninyi mkiyatenda.”
Mkiyajua hayo heri ninyi mkiyatenda!
Rev. Innocent Kamote
Mkuu wa Wajenzi mwenye Hekima!