Ijumaa, 28 Aprili 2017

Kazi za Roho Mtakatifu katika Kanisa!


Andiko la Msingi: Matendo 1:8Lakini mtapokea nguvu, akiisha kuwajilia juu yenu Roho Mtakatifu; nanyi mtakuwa mashahidi wangu katika Yerusalemu, na katika Uyahudi wote, na Samaria, na hata mwisho wa nchi.”


 Hii hapo juu ni picha (symbol) ya Roho Mtakatifu na sio Roho Mtakatifu

Utangulizi.

Hali ya kanisa la leo imekuwa dhaifu kuliko Nyakati za kanisa la Kwanza, Kanisa lilikusudiwa na Mungu kuwa Chombo kikuuu cha ukombozi wa wanadamu Baada ya kazi njema iliyofanywa na Yesu Msalabani, Mungu analitegemea kanisa kuwa kama Waamuzi, watetezi, wakombozi, makuhani, wafalme na askari wa mstari wa mbele katika kuwatetea wanyonge, walioonewa na waliosetwa katika vifungo vya Ibilisi, na kukemea uovu, kuikosoa serikali na kuonyesha njia kwa ulimwengu!

Luka 4: 18-19Roho wa Bwana yu juu yangu, Kwa maana amenitia mafuta kuwahubiri maskini habari njema. Amenituma kuwatangazia wafungwa kufunguliwa kwao, Na vipofu kupata kuona tena, Kuwaacha huru waliosetwa, Na kutangaza mwaka wa Bwana uliokubaliwa.”

Kanisa lilipaswa kufanya kazi hizo alkizozitaja Yesu na kuzitabiri Isaya hapo Juu, ikiwa Roho wa Mungu yuko juu yetu, ikiwa ametupaka Mafuta, lakini jiulize leo hii je kazi zinazofanywa na kanisa ndizo hizo hapo juu? Leo kanisa limejaa watu wengi wenye Stresses yaani migandamizo, lina watu wengi wasio waaminifu bila kujali kuwa wako ngazi gani za kiroho, yale ambayo zamani tulikuwa tunayaona na kuyashuhudia yakifanywa na watu tuliowaita Mataifa watu wasiomjua Mungu, tuliokuwa tukiwalilia waokolewe, wamjue Mungu wamgeukie Mungu sasa ndio yanafanywa na Kanisa, Je ni mara ngapi kanisa limekaa kimya watu wanapoonewa, Mauaji yanapotokea Duniani, vita vinavyoendelea, matishio ya umwagikaji wa damu na dhuluma za kila aina je leo ni nani anaifanya kazi hii? Nani anasimamia haki za binadamu zinazoendana sawa na Neno la Mungu? Kwa nini tumefikia hapa tulipofikia? Kuna na mambo mengi sana sitaki kuyazungumza hapa lakini wewe unayajua kuhusu hali ya kanisa la leo! Ni ya kushangaza, ni kweli ziko huduma za kinabii na mitume na miujiza ambayo inatendeka na najua inatendeka kwa nguvu za Roho Mtakatifu, lakini je uadilifu? Uko? Je Hakuna ulevi, uongo, picha za ngono, chuki, uadui, uchawi, ushirikina, masengenyo, uasherati na zinaa, je hatutoi muda mwingi kwa simu zetu, tablets, na laptop, zaidi kuliko kwa Mungu na familia zetu, hali ni mbaya mno sasa, Turudi kukazia kazi za Roho Mtakatifu ndani ya kanisa, tutajifunza somo hili kwa kuzingatia vipengele viwili vifuatavyo:-

1.       Roho Mtakatifu ni Nani?

2.       Kazi za Roho Mtakatifu Katika ya Kanisa

Roho Mtakatifu Ni nani?

Katika Maandiko Roho Mtakatifu anaelezewa vema kama Nafsi kamili  inayojitegemea yeye ni BWANA yaani ni Mungu 2Wakoritho 3:17-18 17. Basi 'Bwana' ndiye Roho; walakini alipo Roho wa Bwana, hapo ndipo penye uhuru. Lakini sisi sote, kwa uso usiotiwa utaji, tukiurudisha utukufu wa Bwana, kama vile katika kioo, tunabadilishwa tufanane na mfano uo huo, toka utukufu hata utukufu, Waebrania  9:14 Roho Mtakatifu ni wa Milele tunaelezwa katika maandiko “basi si zaidi damu yake Kristo, ambaye kwamba kwa Roho wa milele alijitoa nafsi yake kwa Mungu kuwa sadaka isiyo na mawaa, itawasafisha dhamiri zenu na matendo mafu, mpate kumwabudu Mungu aliye hai?” kuwepo milele ni sifa ya uungu, 1Petro 1:2, Roho Mtakatifu ni Mungu kama ilivyo kwa Baba na Mwana kwa msingi huo hatupaswi kumfikiri Roho mtakatifu kama nguvu tu au hamasa Fulani, ana sifa za nafsi anafikiri, Warumi 8:27 ana hisia Warumi 15:30 ana maamuzi 1Wakoritho 12:11 na ana uwezowa kupenda na kufurahia ushirika , alitumwa na Mungu Baba kuleta uwepo wa kiungu kwa washirika ili tufurahie ushirika wetu na Kristo Yohana 14:16-18,26, kwaajili ya hayo Kanisa linapaswa kukumbuka kuwa Roho ni Mungu na ni nafsi na nilazima tuhakikisha anaunganishwa mioyoni mwetu, na kuwa anastahili kuabudiwa kupendwa na kusikilizwa Marko 1:11

Kazi za Roho Mtakatifu katika Kanisa.

1.       Yeye ndio njia ya wokovu anayetushawishi kwa habari ya haki dhambi na hukumu Yohana 16:7-8 Sasa basi ni vigumu kwa kanisa kujisikia hukumu na kufa kwa dhamiri kama Roho Mtakatifu hapewi nafasi ya kutosha katika kuifanya kazi ya kutuhukumu kwa habari ya dhambi, kutuonyesha kuna hukumu kubwa ijayo endapo hatutatubu na kutushuhudia namna ya kutenda haki.
2.       Anafunua kweli kuhusu Kristo Yohana 14:16,26,
3.       Anatuzaa kwa upya Yohana 3:3-6
4.       Anatufanya washirika wa mwili wa Kristo 1Wakoritho 12:13
5.       Anatutakasa  Warumi 8:9, IWakoritho 6:19
6.       Anatuthibitishia kuwa sisi ni wana wa Mungu Warumi 8:16
7.       Anatusaidia katika kuabudu Matendo 8:26-27
8.       Anatufanya tumtukuze Yesu Kristo Wagalatia 5:22-23,1Petro
9.       Anazalisha neema ya Kristo inayotufanya tuwe na sifa zinazomtukuza Kristo Wagalatia 5:22-23, 1Petro 1:2
10.   Ni Mwalimu  na hutuongoza katika kweli yote  Yohana 16: 13, 14:26, 1Wakoritho 2:9-16
11.   Aanamfunua Yesu kwetu na kutuongoza katika kuwa na ushirika na Yeye Yohana 14:16-18,16:14
12.   Anapanda upendo wa Mungu siku zote ndani yetu  Warumi 5:5
13.   Anatupa Furaha faraja na msaada Yohana 14:16, 1Thesalonike 1:6
14.   Ni njia ya huduma na hututia nguvu kwaajili ya huduma, shuhuda na utangazaji wa Neno la Mungu Matendo 1:8, 4:31 na hutenda miujiza Matendo 2:43;3:2-8, 5:15, 6:8, 10:38
15.   Anatoa Karama za Roho kwa kusudi la kulijenga Kanisa 1Wakoritho 12-14
16.   Analijenga Kanisa Waefeso 2:22, anatia moyo kuabudu Wafilipi 3:3
17.   Anaongoza katika Umisheni Matendo 13:2, anateua waamini Matendo 20:28
18.   Anapaka Mafuta watumishi Matendo 2:4 1Wakoritho 2:4
 
Hitimisho!
Kama ikiwa Roho wa Mungu hufanya kazi hizo zote kanisa halipaswi kumdharau, upungufu mkubwa unaolikumba kanisa la leo unatokana na sababu tu za kumzimisha Roho Mtakatifu, Ni lazima kanisa limpe Roho Mtakatifu kipaumbele kama linataka kuwa hai nnapozungumza kanisa namaanisha kila mtu aliyeokolewa anayemwamini Yesu anapaswa kuzingatia haya ili Kazi za Mungu ziweze kufanyikakatika kiwango ambacho Mungu amekikusudia na sio chini ya kiwango.

Mkuu wa Wajenzi mwenye Hekima

Rev. Innocent Kamote. 0718990796

Jumanne, 18 Aprili 2017

Malaika wa Pasaka!



Mstari wa Msingi: Marko 16:1-8, Mathayo 28:1-10

Hata sabato ilipokwisha, ikipambazuka siku ya kwanza ya juma, Mariamu Magdalene, na Mariamu yule wa pili, walikwenda kulitazama kaburi. Na tazama, palikuwa na tetemeko kubwa la nchi; kwa sababu malaika wa Bwana alishuka kutoka mbinguni, akaja akalivingirisha lile jiwe akalikalia. Na sura yake ilikuwa kama umeme, na mavazi yake meupe kama theluji. Na kwa kumwogopa, wale walinzi wakatetemeka, wakawa kama wafu. Malaika akajibu, akawaambia wale wanawake, Msiogope ninyi; kwa maana najua ya kuwa mnamtafuta Yesu aliyesulibiwa. Hayupo hapa; kwani amefufuka kama alivyosema. Njoni, mpatazame mahali alipolazwa. Nanyi nendeni upesi, mkawaambie wanafunzi wake, Amefufuka katika wafu. Tazama, awatangulia kwenda Galilaya; ndiko mtakakomwona. Haya, nimekwisha waambia. Wakaondoka upesi kutoka kaburini, kwa hofu na furaha nyingi, wakaenda mbio kuwapasha wanafunzi wake habari.  Na tazama, Yesu akakutana nao, akisema, Salamu! Wakakaribia wakamshika miguu, wakamsujudia. Kisha Yesu akawaambia, Msiogope; enendeni, mkawaambie ndugu zangu waende Galilaya, ndiko watakakoniona.


              
Utangulizi:

Inaonekana wazi wakati wote Mungu anapokuwa na Tangazo muhimu sana kwa wanadamu, hutuma ujumbe wake kupitia Malaika, wakati mwingine Malaika wa habari muhimu alijitambulisha kwa jina na wakati mwingine Hakujitambulisha, vyovyote vile iwavyo malaika hao walileta ujumbe Muhimu kwa wanadamu mfano:- 

·         Mungu alituma Malaika kutangaza kuzaliwa kwa Samson Waamuzi 13
·         Mungu alituma Malaika kutangaza kuzaliwa kwa Yohana Mbatizaji Luka 1
·         Mungu alituma Malaika kutangaza kuzaliwa kwa Yesu Kristo Luka 2:8-11
·         Mungu alituma Malaika kushughulika na tatizo la Sodoma na Gomora Mwanzo 19
·         Mungu alimtuma Malaika wa Pasaka wakati wa Ukombozi wa wana wa Israel Misri 12:29

·     Na Mara hii Yesu anapofufuka Malaika wa Pasaka anakuja tena akiwa na ujumbe mzito ambao tutachukua Muda kuutafakari leo.

Malaika wa Pasaka anawatokea kinamama walikuja Kaburini wakiwa wamekata tamaa na wenye fadhaa kubwa sana, walitoka wakiwa hawajua hata ni nani atakayewaondolea jiwe waendelee na kazi ya kupaka mafuta mwili wa Yesu, lilikuwa ni jambo la hatari na lenye kuogopesha mno, lakini Malaika wa Pasaka alikuwa na ujumbe muhimu sana 

1.       Aliwaambia Msiogope.
Inawezekana kina mama waliokwenda Kaburini walishituka zaidi walipoona kijana huyu mwenye mavazi meupe, na waliogopa mno lakini ujumbe wa kwanza wanaoupokea kutoka kwa malaika wa pasaka ni kutokuogopa Mungu wakati wote anataka watu wake wasiogope na wawe na amani, wakati wote haijalishi tunazungukwa na mazingira ya namna gani, Malaika hakutaka kina mama na dunia nzima kwa ujumla itawaliwe na Hofu, hofu ni adui mkuu wa amani, kila mtu anayesheherekea Pasaka anapaswa kuwa Mbali na Hofu, Kama mauti ilimpata Yesu Kristo naye amefufuka hatupaswi kuogopa tena Milele Ufunuo 1:17-18, 2Timotheo 1:3, 8, Dunia ya leo imejawa na Hofu, Huko Syria hivi Karibuni Marekani imepiga Bomu kubwa sana kubwa mno, hali ya hofu inaongezeka , Hapa nchini kule Pwani Polisi kumi wameuawa ambao ni walizni wa amani nchini hii inaongeza Hofu, Kule Korea Kaskazini na Marekani wamekuwa na mikwara ya kustaajabisha wakitaka kupigana hali hizi zote zinaoneza hofu duniani na kuifanya Dunia isiwe mahali pa Amani ni lazima jitihada zifanyike katika kuhakikisha Amani inatawala Duniani na watu wanaondoka katika maisha ya hofu.

2.       Amefufuka Katika wafu.
Malaika anataka kuthibitisha kuwa Yesu alisulubiwa, na alikufa na kuwa amefufuka maana yake yu hai, Ufunuo 1:17-18 Yesu yu Hai milele na milele, kama kuna jambo ambalo shetani hapendi kulisikia ni ushahidi ulio wazi kuwa Yesu amefufuka, hii ndio tofauti yake na waanzilishi wote wa dini na falsafa mbalimbali duniani, wote waliandika historian a wakapita sivyo ilivyo kweke Yesu Kristo yeye yuko hai milele, ulikuwa ni ujumbe wa kutia moyo kwa kina mama hawa walikuwa wamenunua mafuta ya kuupaka mwili wa Yesu usizoe, aendelee kuwepokuwepo kaburini, Lakini Neno la malaika lilikuja kuondoa mashaka kwao na kuwajulisha kuwa hata mafuta yenu ya kumpaka Merehemu hayana kazi tena huyu mwanamume yu hai.Aidha malaika alikuwa amewakumbusha Maneno aliyoyasema Yesu kuwa atafufuka hii maana yake ni kuwa Yesu aliitimiza ahadi, viongozi wazuri ni wale wanaotimiza ahadi zao mara baada ya Uchaguzi kama ilivyo kwa Pombe Joseph Magufuli anatimiza ahadi nyingi sana alizowaahidi watanzania, lakini nitoe wito kwake kuendelea kudhibiti mfumo wa Bei ya chakula kwani imepanda mmno na kipato cha watanzania hakitoshelezi katika kukabiliana na kupanda kwa unga na vyakula vinginevyo.

3.       Hayuko Hapa
Malaika aliwaambia wanawake hawa wawe watalii wa kwanza wa kulitembelea Kaburi la Yesu lililotupu, aliwaambia Patazameni mahali walipomuweka, hata leo unaweza kwenda kupatazama mahali walipomuweka Hayupo tena, yuko Hai, Kaburi lake ni ushahidi wazi hata leo kuwa Yesu Kristo amefufuka na tayari yuko busy na majukumu ya kutuombea kama kuhani mkuu

4.       Nendeni Mkwawaambie wanafunzi wake na Petro
Habari njema kwa wanafunzi wote wa Yesu. Lakini pia maalumu kwa Petro, Petro na Yesu walikuwa tayari wameachana pabaya Petro alikuwa tayari amemkana Yesu Mara tatu wakati anasulubiwa Malaika ametumwa kulete ujumbe wa ufufuo kwa wanafunzi wote wa Yesu na maalumu kwa Petro pia, Mungu alitaka kuthibitisha kuwa ameshamsamehe Petro kabisa na kuwa sasa ana uhusiano naye mkubwa na wa kipekee zaidi, Habari njema za ufufuo zinawagusa hata wale ambao walikuwa wamemkana Yesu, Yesu kipakee anaonyesha kuhusika na rafiki zake wote na hata wale waliomkataa kivitendo na kwa kiapo

Malaika alikuwa na ujumbe uliobeba Kuondoa Hofu, Kuleta Matumaini, Msamaha na uthibitisho kuwa tutamuona Yesu aliyefufuka, Kila kiongozi wa kisiasa kuanzia ngazi ya kata anapaswa kuhakikisha wanainchi wanaishi mbali na Hofu, tuache kuwatisha wanainchi, Lazima kila kiongozi alete habari za matumaini na kututhibitishia hali halisi ya tumaini hilo Yesu alikuwa ni kiongozi aliyetoka tunmaini na alilithibitisha, aliposema yeye ni ufufuo na uzima alifuua wafu lakini pia alifufuka kwelikweli, aliweza kusamehe na kuwahesabu wale waliomkosea kama rafiki maalumu na sio maadui zake, viongozi wa leo hawapaswi kujenga hali ya uadui na raia wake, ahadi zake zilikuwa za kweli hakutoa matumaini hewa.

Na mkuu wa Wajenzi Mwenye Hekima
Rev. Innocent Kamote.

Jumatatu, 3 Aprili 2017

Mwamba wenye Imara.

Andiko: 1Wakoritho 10:4 Biblia inasema “wote wakanywa kinywaji kile kile cha roho; kwa maana waliunywea mwamba wa roho uliowafuata; na mwamba ule ulikuwa ni Kristo.”

 Mji uliochongwa katika Mwamba huko Jordan unajulikana kama mji wa Petra yaani Mwamba

Utangulizi:

Ilikuwa mwaka wa 1763 wakati Mchungaji Rev.Augustus  Montague Toplady, Muhubiri wa Injili kutoka kijiji cha Blagdon Huko Mendip Hill Uingereza, alipokuwa akisafiri kwa shughuli za injili, alikumbwa na dhoruba kali sana njiani alijaribu kutafuta hifadhi katika moja ya miamba na kufanikiwa kuwa salama na ndipo baadaye alitunga wimbo MWAMBA WENYE IMARA au MWAMBA ULIOPASUKA ambao ni moja ya nyimbo kuu na za Muhimu sana kwa waanglikan na umekuwa maarufu katika tenzi za rohoni namba 58 na nyimbo za injili 30, wimbo huu ulichapishwa kwa mara ya kwanza mwaka 1775 na gazeti moja la injili lililojulikana kama The gospel Magazine. Wimbo ulipendwa sana na Prince Albert ambaye aliagiza wimbo huo upigwe siku atakapokufa na ndipo ukawa maarufu sana wakati wa misiba hata ingawaje wimbo huu unamzunguzia Yesu kama Mwamba.
Mwamba wenye imara,
Kwako nitajificha,
Maji hayo na damu,
Yaliyotoka humu,
Hunisafi na dhambi,
Hunifanya mshindi.

Kwa kazi zote pia,
Sitimizi sheria,
Nijapofanya bidii,
Nikilia na kudhii,
Hayaishi makosa,
Ndiwe wa kuokoa. 

Sina cha mkononi,
Naja msalabani,
nili tupu, Nivike,
Ni mnyonge, nishike,
Nili mchafu naja,
Nioshe nisijafa.

Nikungojapo chini,
Na kwenda kaburini,
Nipaapo mbinguni,
Na kukwona enzini,
Roho yangu na iwe,
Rahani mwako wewe.


Mtunzi wa wimbo huu aliokoa maisha yake katika mwamba! Na kwa vile alikuwa muhubiri alielewa wazi kuwa Mwamba ulimwakilisha Yesu Kristo, Katika majira haya ya Pasaka ni muhimu kwetu kurudi katika maandiko na kutafakari kwa kina kwa nini Yesu anaitwa Mwamba? Watakatifu waliotutangulia walimfananisha Mungu na mwamba.

Biblia inamtaja wazi Mungu wetu kuwa ni Mwamba wa wokovu wetu

1.       Zaburi ya 18:2 Bwana ni jabali langu, na boma langu, na mwokozi wangu, Mungu wangu, mwamba wangu ninayemkimbilia, Ngao yangu, na pembe ya wokovu wangu, na ngome yangu.

2.       Zaburi ya 62:1-2 Nafsi yangu yamngoja Mungu peke yake kwa kimya, Wokovu wangu hutoka kwake.  Yeye tu ndiye mwamba wangu na wokovu wangu, Ngome yangu, sitatikisika sana

3.       Zaburi ya 95: 1 Njoni, tumwimbie Bwana, Tumfanyie shangwe mwamba wa wokovu wetu.

Neno mwamba katika Biblia ya Kiebrania linatajwa kwa maneno makuu mawili yaani TSUR ambalo maana yake ni gema au pande kubwa la jiwe, na neno lingine ni SELA ambalo maana yake ni mlima au Jabali au ngome ya Jiwe, Kiyunani ni Peter na Petra
 
Kwa hivyo Biblia inapomtaja Kristo kama Mwamba inamaanisha SELA au PETRA Kila mmoja wetu anaweza kujua ujasiri anaojisikia akiwa juu ya mwamba unapokuwa juu ya mwamba au juu ya jabali unaweza kukaa kwa ujasiri, unaweza kurukaruka na hakuna wa kukubabaisha, mwamba huwa hautikisiki, haung’oki, hauogopi dhoruba na kama mtu atashindana na mwamba atavunjika vunjika na kama mtu ataangukiwa na mwamba atasagwasagwa!

Hakuna njia nyingine yoyote ambayo kwa hiyo tunaweza kuwa salama isipokuwa kumtegemea Yesu tu mtuni wa wimbo alionyesha kuwa ni kwa Damu yake yesu tu tunaweza kuwa salama, kwake tunaweza kujificha na kuutegemea ushidni, kazi njema , na matendo mema hayawezi kutuokoa ni zawadi ya Yesu Kristo pekee aliyekufa msalabani kwaajili yetu ndio inayoweza kututhibitishia usalama wetu, kwa jambo lolote lile ni lazima tuweke tegemeo letu kwa Bwana Yesu

Tunaweza kukutana na dhuruba za aina mbalimbali zenye kuhuzunisha Magonjwa na mateso, Matatizo ya kifedha na kiuchumi, Matatizo ya kifamilia, Huzuni na kukata tamaa jambo kubwa na la msingi la kufanya ni kumwangalia Yesu ni kumtegemea ni kujificha kwake yeye ndio nguvu yetu, na kimbilio letu ndiye mwamba imara 

Yeye aliahidi kuwa atalijenga kanisa lake juu ya mwamba na wala malango ya kuzimu hayatalishinda, ushindi ni wetu kama tu tutajificha na kuutegemea Mwamba.  

Mathayo 16: 13-18Basi Yesu akaenda pande za Kaisaria-Filipi, akawauliza wanafunzi wake akasema, Watu hunena Mwana wa Adamu kuwa ni nani? Wakasema, Wengine hunena u Yohana Mbatizaji, wengine Eliya, wengine Yeremia au mmojawapo wa manabii.  Akawaambia, Nanyi mwaninena mimi kuwa ni nani?  Simoni Petro akajibu akasema, Wewe ndiwe Kristo, Mwana wa Mungu aliye hai. Yesu akajibu, akamwambia, Heri wewe Simoni Bar-yona; kwa kuwa mwili na damu havikukufunulia hili, bali Baba yangu aliye mbinguni. Nami nakuambia, Wewe ndiwe Petro, na juu ya mwamba huu nitalijenga kanisa langu; wala milango ya kuzimu haitalishinda.”

Rev. Innocent Kamote
Mkuu wa Wajenzi mwenye Hekima.