Jumanne, 20 Septemba 2022

Ukikubali kuwa mtumwa utatumikiwa Daima !


1Wafalme 12:6-7 “Mfalme Rehoboamu akataka shauri kwa wazee waliokuwa wakisimama mbele ya Sulemani, baba yake, alipokuwa hai, akasema, Mwanipa shauri gani ili niwajibu watu hawa?  Wakamwambia wakasema, Ukikubali kuwa mtumishi wa watu hawa leo, na kuwatumikia, na kuwajibu, na kuwapa maneno mazuri, basi watakuwa watumishi wako daima.”



Utangulizi:

Mojawapo ya maombi yanayompendeza sana Mungu ni pamoja na kuomba Hekima, Mfalme Suleimani mara alipotawazwa kuwa mfalme wa Israel, Mungu alimtokea na kumtaka amuombe lolote alitakalo, katika namna ya kushangaza sana Mfalme Suleimani aliomba Hekima jambo ambalo lilimpendeza sana Mungu hata akamjalia na mambo mengine mengi sana ambayo hakuyaomba ona:-

1Wafalme 3:5-13 “Na huko Gibeoni Bwana akamtokea Sulemani katika ndoto ya usiku; Mungu akamwambia, Omba utakalo nikupe. Sulemani akasema, Umemfanyia mtumwa wako Daudi baba yangu fadhili kuu, kadiri alivyoenenda mbele zako katika kweli, na katika haki, na katika unyofu wa moyo pamoja nawe; nawe umemwekea na fadhili hii kubwa, maana umempa mwana wa kuketi kitini pake kama ilivyo leo. Na sasa, Ee Bwana, Mungu wangu, umenitawaza niwe mfalme mimi mtumwa wako badala ya Daudi baba yangu; nami ni mtoto mdogo tu; sijui jinsi inipasavyo kutoka wala kuingia. Na mtumwa wako yu katikati ya watu wako uliowachagua, watu wengi wasioweza kuhesabiwa, wala kufahamiwa idadi yao, kwa kuwa ni wengi. Kwa hiyo nipe mimi mtumwa wako moyo wa adili niwahukumu watu wako, na kupambanua mema na mabaya; maana ni nani awezaye kuwahukumu hawa watu wako walio wengi? Neno hili likawa jema machoni pa Bwana, ya kuwa Sulemani ameomba neno hili. Mungu akamwambia, Kwa kuwa umeomba neno hili, wala hukujitakia maisha ya siku nyingi; wala hukutaka utajiri kwa nafsi yako; wala hukutaka roho za adui zako; bali umejitakia akili za kujua kuhukumu; basi, tazama, nimefanya kama ulivyosema. Tazama, nimekupa moyo wa hekima na wa akili; hata kabla yako hapakuwa na mtu kama wewe, wala baada yako hatainuka mtu kama wewe. Na mambo yale usiyoyaomba nimekupa, mali na fahari, hata hapatakuwa na mtu katika wafalme kama wewe, siku zako zote.”

Kila siku katika maisha yetu tunakabiliwa na swala la kufanya uamuzi, Hakuna jambo gumu sana duniani kama kufanya uamuzi, maamuzi yetu tunayoyafanya leo yanaweza kuwa na faida kubwa sana katika siku zetu zote za maisha yetu na ya watu wengine, lakini vilevile yanaweza kutugharimu na kusababisha machungu katika maisha yetu au hata na ya wengine kwa hiyo ni muhimu sana kumuomba Mungu atupe Hekima.

Yakobo 1:5 “Lakini mtu wa kwenu akipungukiwa na hekima, na aombe dua kwa Mungu, awapaye wote, kwa ukarimu, wala hakemei; naye atapewa.”

Katika kifungu cha maandiko ya msingi, tulichosoma tunamuona Mwana wa mfalme Sulemani aliyeitwa Rehoboamu akiwa anakabiliwa na wakati wa kufanya maamuzi kwa mustakabali wa taifa lake mapema tu katika siku za mwanzoni mwa utawala wake.

1Wafalme 12:1-5 “Rehoboamu akaenda Shekemu; maana Israeli wote walikuwa wamekwenda Shekemu, ili kumfanya mfalme. Ikawa Yeroboamu mwana wa Nebati alipopata habari (maana alikuwa akaliko Misri, huko alikokimbilia awe mbali na mfalme Sulemani; Yeroboamu akakaa huko Misri, wakapeleka watu kwenda kumwita); basi Yeroboamu na jamii yote ya Israeli wakaenda, wakamwambia Rehoboamu, wakasema, Baba yako alilifanya zito kongwa letu; basi sasa utupunguzie utumwa mzito tuliotumikishwa na baba yako, na lile kongwa zito alilotutwika, nasi tutakutumikia. Akawaambia, Enendeni zenu hata siku ya tatu, kisha mnirudie tena. Watu wakaenda zao.”

Wana wa Israel wanaonekana ya kuwa walikuwa tayari kabisa kumtumikia mfalme Rehoboamu baada ya baba yake Suleimani, lakini walikuwa na ombi kwamba wawarahisishie maisha maana wakati wa baba yake hali ilikuwa ngumu sana walielemewa na kodi na utumwa mzito uliowanyima furaha, Suleimani alikuwa amewatumikisha watu sana kwa utumwa mzito na Kodi kwaajili ya fahari ya ufalme wake, Mfalme Rehoboamu aliwapa Muda ili kwamba aweze kulitafakari ombi lao, jambo hili au hatua hii ilikuwa njema kwani hakufanya haraka alikuwa na utulivu na hii ni hatua nzuri kila wakati tunapotaka kufanya maamuzi, hatupaswi kufanya maamuzi kwa kufuata mihemko, ni muhimu kutulia na ikiwezekana kuwa na wakati wa kumuomba Mungu ili kwamba atupe hakima ya kufanya maamuzi mema yanayokusudiwa, Mungu akitupa hekima yake tutakuwa na mafanikio makubwa sana yaani matunda mema kwa sababu hekima ya Mungu ni safi, ya amani, ya upole, na inasikiliza watu hekima hii ina rehema, na ina matunda mema haina fitina wala haina unafiki imetajwa hivyo katika maandiko;-

Yakobo 3:17-18 “Lakini hekima itokayo juu, kwanza ni safi, tena ni ya amani, ya upole, tayari kusikiliza maneno ya watu, imejaa rehema na matunda mema, haina fitina, haina unafiki. Na tunda la haki hupandwa katika amani na wale wafanyao amani.”

Tunapotafakari haya tutaliangalia somo hili katika vipengele vitatu vifuatavyo:-

1.       Ushauri wa wazee na ushauri wa vijana

2.       Umuhimu wa kufanya maamuzi yenye busara

3.       Ukikubali kuwa mtumwa utatumikiwa Daima

Ushauri wa wazee na ushauri wa vijana.

Kuna kitu cha kujifunza tunapoangalia maamuzi yaliyofanywa na mfalme Rehoboamu, Maamuzi yake yanaletwa kwetu na neno la Mungu ili tuweze kujifunza maswala halisi yanayoweza kujitokeza kwetu katika maisha  Mfalme Rehoboamu alipotulia ili atake ushauri, alipata ushauri kutoka katika makundi makuu mawili, kundi la kwanza lilikuwa kundi la wazee hawa walikuwa ni watu waliokuwa na uzoefu na ujuzi (Experience) walikuwa wameona utawala uliopita wa wakati wa baba yake walijua mazuri na machungu ya utawala huo, kwa kawaida Biblia inapotaja wazee wakati mwingine huwa inazungumzia UZOEFU hawa walitoa ushauri wao  kama hivi ona

 1Wafalme 12:6-7 Mfalme Rehoboamu akataka shauri kwa wazee waliokuwa wakisimama mbele ya Sulemani, baba yake, alipokuwa hai, akasema, Mwanipa shauri gani ili niwajibu watu hawa? Wakamwambia wakasema, Ukikubali kuwa mtumishi wa watu hawa leo, na kuwatumikia, na kuwajibu, na kuwapa maneno mazuri, basi watakuwa watumishi wako daima.”

Kundi hili ni kundi la watu wanaojua wapi tunatoka na wapi tunakwenda, maandiko yanaonyesha kuwa walikuwa ni washauri pia wa Mfalme Suleimani, maandiko yanasema waliokuwa wakisimama mbele ya Sulemani alipokuwa hai, hawa waliona ukatili aliokuwa nao Sulemani na ukali wake hunda kuna mambo walishauri na Sulemani kwa ubabe wake alikataa, na sasa anapokuja mfalme mpya walimshauri kwamba akubali kuwa mtumwa yaani mtumishi awajali watu awatumie watu lakini vilevile azungumze nao vizuri, awape majibu akutane na haja za mioyo yao, na kuwapa maneno mazuri, walimwambia akifanya hivyo watu hawa watamtumikia daima.  

Kundi la Pili lilikuwa kundi la vijana, vijana katika lugha ya kinabii ni watu wasio na uzoefu, hawana ujuzi wa kutosha wa kupambanua mambo, wao walikuwa ni machipukizi bado hawana mizizi kundi hili wao walimpa mfalme ushauri wa kuongeza ukatili na kutokuwahurumia watu

1Wafalme 12:8-11 “Lakini akaliacha shauri lile la wazee, walilompa, akataka shauri kwa wale vijana waliokua pamoja naye, na kusimama mbele yake. Akawaambia, Mwanipa shauri gani ili tuwajibu watu hawa, waliosema nami, wakinena Utufanyie jepesi kongwa lile alilotutwika baba yako? Na wale vijana waliokua pamoja naye wakamwambia, wakasema, Uwaambie hivi watu wale waliokuambia, wakisema, Baba yako alilifanya zito kongwa letu, bali wewe utufanyie jepesi, uwaambie hivi, Kidole changu cha mwisho ni kinene kuliko kiuno cha baba yangu. Basi kama vile baba yangu alivyowatwika kongwa zito, mimi nitaongeza kongwa lenu; baba yangu aliwapiga kwa mijeledi, bali mimi nitawapigeni kwa nge.”

Mfalme Rehoboamu kwa bahati mbaya alifuata ushauri wa vijana maana yake alifuata ushauri wa watu wasio na uzoefu, wajanja wajanja ambao kimsingi walikuwa wakitarajia nafasi kadhaa katika utawala mpya hivyo wasingekuwa na jipya zaidi ya kumpamba mfalme na kumpa maneno ambayo walifikiri yangeweza kuwa na tija katika jamii matokeo yake wana wa Israel waligawanyika makundi makundi na inchi ya Israel ikapoteza umoja na kuvunjika katika falme mbili

1Wafalme 12:12-16 “Basi, Yeroboamu na watu wote wakamfikia Rehoboamu siku ya tatu, kama mfalme alivyoamuru, akisema, Mnirudie siku ya tatu. Mfalme akawajibu watu wale kwa ukali, akaliacha shauri lile wazee walilompa; akawajibu kama vile walivyomshauri vijana, akasema, Baba yangu alilifanya zito kongwa lenu, bali mimi nitaongeza kongwa lenu; baba yangu aliwapiga kwa mijeledi, bali mimi nitawapigeni kwa nge. Basi mfalme hakuwasikia wale watu; maana jambo hili lilitoka kwa Bwana, ili alitimize neno lake, Bwana alilomwambia Yeroboamu mwana wa Nebati kwa kinywa cha Ahiya Mshiloni. Basi Israeli wote walipoona ya kuwa mfalme hakuwasikia, hao watu walimjibu mfalme, wakasema, Tuna sehemu gani katika Daudi? Wala hatuna urithi katika mwana wa Yese. Haya! Nendeni zenu hemani kwenu, enyi Israeli; sasa itunze nyumba yako mwenyewe, Ee Daudi. Hivyo Israeli wakaenda zao hemani kwao.”

Umuhimu wa kufanya maamuzi yenye busara

Ni jambo la kusikitisha sana kuwa Nchi ya Israel iligawanyika na watu walivunjika Moyo, mfalme hakuwajibu watu kwa upole na badala yake aliwajibu watu kwa ukali na watu wakavunjika moyo kila mmoja akarejea nyumbani kwake,  Siku zote katika maisha yetu hatuna budi kuhakikisha ya kuwa tunafanya maamuzi ambayo yanampendeza Mungu maamuzi ambayo kwa namna yoyote ile hayatakuja yawaumize watu na kuwakatisha tamaa, tusifanye uamuzi wowote wenye kuaibisha watu au kudhalilisha, au kuumiza, tusifanye kwa mihemko yetu wala kwa ubinafsi wetu wala kwa kutaka makuu, Mungu anatutaka watu wote tuwe na maamuzi yenye busara, watu wa Mungu hawapaswi kuwa kama watu wa dunia hii, katika kanuni za kimungu kuwatumikia watu ndio hatua ya juu zaidi itakayotupa heshima kwa Mungu, Bwana Yesu ametufundisha kuwa namna hiyo

Mathayo 20:25-28 “Lakini Yesu akawaita, akasema, Mwajua ya kuwa wakuu wa Mataifa huwatawala kwa nguvu, na wakubwa wao huwatumikisha. Lakini haitakuwa hivyo kwenu; bali mtu ye yote anayetaka kuwa mkubwa kwenu, na awe mtumishi wenu; na mtu ye yote anayetaka kuwa wa kwanza kwenu na awe mtumwa wenu; kama vile Mwana wa Adamu asivyokuja kutumikiwa, bali kutumika, na kutoa nafsi yake iwe fidia ya wengi.”

Kumbe ni kanuni ya kibiblia kabisa ya kuwa  tunapaswa kuwatumikia watu kwa maana nyingine tuwe wanyenyekevu na jambo hili litatupa faida kubwa sana katika maisha yetu, Wazee walikuwa wamemshauri Rehoboamu namna njema ya kufaulu walimtaka awe mnyenyekevu kwa watu, awe mpole azungumze nao kwa amani awe mtumwa na kuwa watu wangemtumikia daima, kumbe katika maisha yetu tukitaka kufanikiwa tukubali kuwa watumwa, tujinyenyekeze, tutii wazee, tusikilize wakubwa, tusikilize walimu, tusikilize wazazi, na walezi, tusikilize wale wenye uzoefu wanatuambia nini  na wakati wote tukatae hali ya kujifanya mabwana:-

1Petro 5: 1-3 “Nawasihi wazee walio kwenu, mimi niliye mzee, mwenzi wao, na shahidi wa mateso ya Kristo, na mshirika wa utukufu utakaofunuliwa baadaye; lichungeni kundi la Mungu lililo kwenu, na kulisimamia, si kwa kulazimishwa, bali kwa hiari kama Mungu atakavyo; si kwa kutaka fedha ya aibu, bali kwa moyo. Wala si kama wajifanyao mabwana juu ya mitaa yao, bali kwa kujifanya vielelezo kwa lile kundi.”

Ukikubali kuwa mtumwa utatumikiwa Daima!.

Huu ndio ushauri mwema kutoka katika mapenzi ya Mungu, wazee walimshauri Rehoboamu kwamba ukikubali kuwa mtumishi wa watu hawa watakutumikia daima, hii ndio kanuni ya msingi ya kibiblia na ina faida nyingi sana kwa mujibu wa maandiko;-

1.       Ukijinyenyekesha utainuliwa juu sana, unapokubali kuwa mtumwa Mungu atakuinua juu mno utapanda katika viwango na watu wote watakutumikia ona Wafilipi 2:5-11 “Iweni na nia iyo hiyo ndani yenu ambayo ilikuwamo pia ndani ya Kristo Yesu; ambaye yeye mwanzo alikuwa yuna namna ya Mungu, naye hakuona kule kuwa sawa na Mungu kuwa ni kitu cha kushikamana nacho; bali alijifanya kuwa hana utukufu, akatwaa namna ya mtumwa, akawa ana mfano wa wanadamu;  tena, alipoonekana ana umbo kama mwanadamu, alijinyenyekeza akawa mtii hata mauti, naam, mauti ya msalaba. Kwa hiyo tena Mungu alimwadhimisha mno, akamkirimia Jina lile lipitalo kila jina; ili kwa jina la Yesu kila goti lipigwe, la vitu vya mbinguni, na vya duniani, na vya chini ya nchi; na kila ulimi ukiri ya kuwa YESU KRISTO NI BWANA, kwa utukufu wa Mungu Baba. Hii ni kanuni huru ya kibiblia Zaburi 147:6 “Bwana huwategemeza wenye upole, Huwaangusha chini wenye jeuri.” Bwana wetu Yesu Kristo alikubali kuwa mtumwa, aliwatumikia watu, kumbuka alikuwa sawa na Mungu alikini alijinyenyekeza moyo wake ulijikita katika kumtumikia Mungu na watu wake na hivyi Mungu alimuinua juu sana na kumpa jina lipitalo majina yote na kutukuzwa sana mbinguni na duniani.

2.       Kujinyenyekeza kunaongeza Neema ya Mungu, 1Petro 5:5-6 “Vivyo hivyo ninyi vijana, watiini wazee. Naam, ninyi nyote jifungeni unyenyekevu, mpate kuhudumiana; kwa sababu Mungu huwapinga wenye kiburi, lakini huwapa wanyenyekevu neema. Basi nyenyekeeni chini ya mkono wa Mungu ulio hodari, ili awakweze kwa wakati wake;” Hakuna jambo baya duniani kama kupungukiwa neema, Mungu wetu ana upendo mkubwa sana aukipata neema mbele zake utafanikiwa katika maisha yako, lakini kiburi ni sumu ya neema, kama tukishindwa kujinyenyekesha haraka sana Mungu ataondoa neema yake kwetu! Na hivyo tutajisikia vibaya na kupatwa na aibu.

3.       Kujinyenyekeza kunaleta kukubaliwa na kujikweza kunaleta kukataliwa Luka 18:9-14 “Akawaambia mfano huu watu waliojikinai ya kuwa wao ni wenye haki, wakiwadharau wengine wote. Watu wawili walipanda kwenda hekaluni kusali, mmoja Farisayo, wa pili mtoza ushuru. Yule Farisayo akasimama akiomba hivi moyoni mwake; Ee Mungu, nakushukuru kwa kuwa mimi si kama watu wengine, wanyang'anyi, wadhalimu, wazinzi, wala kama huyu mtoza ushuru. Mimi nafunga mara mbili kwa juma; hutoa zaka katika mapato yangu yote. Lakini yule mtoza ushuru alisimama mbali, wala hakuthubutu hata kuinua macho yake mbinguni, bali alijipiga-piga kifua akisema, Ee Mungu, uniwie radhi mimi mwenye dhambi. Nawaambia, huyu alishuka kwenda nyumbani kwake amehesabiwa haki kuliko yule; kwa maana kila ajikwezaye atadhiliwa, naye ajidhiliye atakwezwa.” Yakobo 4:10 “Jidhilini mbele za Bwana, naye atawakuza.” 3Yohana 1:9 “Naliliandikia kanisa neno, lakini Diotrefe, apendaye kuwa wa kwanza kati yao, hatukubali.”

4.       Mungu huwasikiliza wanyenyekevu 2Nyakati 34:27 “kwa kuwa moyo wako ulikuwa mwororo, nawe umejinyenyekeza mbele ya Mungu, uliposikia maneno yake juu ya mahali hapa, na juu ya wakaao, ukajinyenyekeza mbele zangu, na kuyararua mavazi yako, na kulia mbele zangu; mimi nami nimekusikia, asema Bwana.”

5.       Unyenyekevu unaleta hekima na kutufanya tukubali kufundishika ona Zaburi 25:9 “Wenye upole atawaongoza katika hukumu, Wenye upole atawafundisha njia yake”. na Mithali 11:2 “Kijapo kiburi ndipo ijapo aibu; Bali hekima hukaa na wanyenyekevu.”

6.       Huepusha hasira ya Mungu na kutupa wokovu ona 2Nyakati 32:26 “Hata hivyo Hezekia akajinyenyekeza kwa ajili ya huku kutukuka kwa moyo wake, yeye na wenyeji wa Yerusalemu, hata haikuwajia hasira ya Bwana siku za Hezekia.” na Zaburi 149:4 “Kwa kuwa Bwana awaridhia watu wake, Huwapamba wenye upole kwa wokovu.

7.       Ukijishusha utakuwa mkubwa katika ufalme wa Mungu Mathayo 18:4 Basi, ye yote ajinyenyekeshaye mwenyewe kama mtoto huyu, huyo ndiye aliye mkuu katika ufalme wa mbinguni.”    

Kama Rehoboamu angejinyenyekeza angeweza kupata thawabu kubwa na nyingi zinazotajwa katika mandiko, Bwana na ampe neema kila mmoja wetu kujifunza umuhimu wa kunyenyekea na kujishusha ili tuweze kuona faida na uzuri wa kanuni za kimungu sawa na namna Mungu anavyokusudia katika Maisha yetu na tukumbuke siku zote ya kuwa ukikubali kuwa mtumwa utatumikiwa Daima.

Rev. Innocent Kamote.

Mkuu wa wajenzi mwenye Hekima!

Alhamisi, 15 Septemba 2022

Kuhani mkuu kwa Mfano wa Melkizedek


Zaburi 110:1-4 “Neno la Bwana kwa Bwana wangu, Uketi mkono wangu wa kuume, Hata niwafanyapo adui zako Kuwa chini ya miguu yako.  Bwana atainyosha toka Sayuni Fimbo ya nguvu zako. Uwe na enzi kati ya adui zako; Watu wako wanajitoa kwa hiari, Siku ya uwezo wako; Kwa uzuri wa utakatifu, Tokea tumbo la asubuhi, Unao umande wa ujana wako. Bwana ameapa, Wala hataghairi, Ndiwe kuhani hata milele, Kwa mfano wa Melkizedeki.”



Utangulizi

Maandiko yanamuonyesha Yesu Kristo kama ni Nabii mkubwa na aliyebora zaidi kuliko Musa, lakini pia ni Kuhani mkuu aliye bora zaidi kwa mfano wa Melkizedeki unaweza kuona poia katika Waebrania 6:20 “alimoingia Yesu kwa ajili yetu, mtangulizi wetu, amekuwa kuhani mkuu hata milele kwa mfano wa Melkizedeki.” Tunapojifunza somo hili kuhani mkuu kwa mfano wa Melkizedeki tutazingatia vipengele vitatu vifuatavyo:-

·         Tofauti ya nabii na kuhani

·         Wajibu wa kikuhani.

·         Kuhani mkuu kwa mfano wa Melkizedeki

Tofauti ya Nabii na kuhani

Neno la Mungu linatufundisha tofauti kubwa iliyoko kati ya nabii na kuhani, kwa kawaida hawa wote ni watumishi wa Mungu, na huwa wanaitwa ama kuteuliwa na Mungu mwenyewe ona Kumbukumbu 18:18 “Mimi nitawaondokeshea nabii miongoni mwa ndugu zao mfano wako wewe, nami nitatia maneno yangu kinywani mwake, naye atawaambia yote nitakayomwamuru.” Unaona ni Mungu ndiye anayeinua nabii na kuweka neno lake ndani yao ili aseme kwa niaba yake na kuwafundisha watu wa Mungu njia zake nan i Mungu mwenyewe anayechagua kuhani ona Waebrania 5:1-4 “Maana kila kuhani mkuu aliyetwaliwa katika wanadamu amewekwa kwa ajili ya wanadamu katika mambo yamhusuyo Mungu, ili atoe matoleo na dhabihu kwa ajili ya dhambi; awezaye kuwachukulia kwa upole wao wasiojua na wenye kupotea, kwa kuwa yeye mwenyewe yu katika hali ya udhaifu; na kwa sababu hiyo imempasa, kama kwa ajili ya watu, vivyo hivyo kwa ajili ya nafsi yake mwenyewe, kutoa dhabihu kwa ajili ya dhambi. Na hapana mtu ajitwaliaye mwenyewe heshima hii, ila yeye aitwaye na Mungu, kama vile Haruni.” Unaweza kuona hawa wote huteuliwa au kuitwa na Mungu, Nabii yeye huchaguliwa na Mungu ili awe msemaji kwa niaba ya Mungu Neno nabii katika Lugha ya kiibrania huwakilishwa kwa maneno makuu matatu ambayo ni NABI, ROEH, na HOZEH

Nabi – Maana yake ni Msemaji, au mtangazaji Hawa ni wasemaji au wanenaji wanaosukumwa na Roho wa Mungu kuyasema mapenzi ya Mungu kwa msukumo na wivu mkali wa kiungu, lakini pia ni walimu wa neno la Mungu kwa ufupi ni wasemaji kwa niaba ya Mungu, ni wasemaji wa Mapenzi ya Mungu

Roeh – Maana yake ni waonaji, au wafunuaji wao hitwa na Mungu na kuwawezesha kuona mambo yaliyofichika na kuyasema au kuonya au kutangaza au kufundisha mapenzi ya Mungu baada ya kufunuliwa na Mungu, mwisho wa siku nao ni wasemaji kwa niaba ya Mungu

Hozeh – Ni msahuri au mwenye hekima ambao kazi yao ni kufikiri na kutoa ushauri kwa niaba ya Mungu kwa watu wake ni wenye uwezo wa kutambua kama ujumbe ni wa kiungu au la walitumika sana kuwashauri wafalme ili watende sawasawa na mapenzi ya Mungu

Katika kiyunani Prophet ni mtu anayezungumza jambo kwa niaba ya mwingine kwa hivyo wao husema au kutafasiri jambo kwa niaba ya Mungu, ili watu wa Mungu wajue mapenzi ya Mungu katika maisha yao hivyo kwa vyovyote vile manabii ni walimu wa neno la Mungu, ni walimu kwa niaba ya Mungu ni wajumbe kwa niaba ya Mungu, Mungu anapotaka kuyafunua mapenzi yake kwa wanadamu.

Kuhani kwa upande mwingine ni mwanaume anayechaguliwa na Mungu kuwawakilisha wanadamu kwa Mungu, wao ni wasemaji wa wanadamu kwa Mungu, wana wana kibali maalumu cha kumfikia Mungu, na kuzungumza au kutenda kwa niaba ya wanadamu kwa Mungu , hata hivyo hii haiachi ukweli kuwa nao ni walimu wa nenola Mungu kwa watu wa Mungu, lakini mafundisho yao ni tofauti nay ale ya manabii, wakati manabii wanakazia uadilifu, hali safi ya kiroho na wajibu wetu kwa Mungu, Makuhani wao hushughulika na njia sahihi za kumuendea Mungu.

Wajibu wa kikuhani.

Huduma ya kikuhani kwa kawaida kihistoria ilianzishwa na Mungu kwa wana wa Israel baada ya kutoka katika inchi ya Misri, baada ya maelekezo ya Mungu kwa Musa katika mlima wa Sinai, Kutoka 28:1 “Nawe umlete Haruni ndugu yako karibu nami, na wanawe pamoja naye, miongoni mwa wana wa Israeli, ili anitumikie katika kazi ya ukuhani. Haruni, na Nadabu, na Abihu, na Eleazari, na Ithamari, wana wa Haruni.” Makuhani hawa walichaguliwa kutoka miongoni mwa wanadamu ili waweze kuwawakilisha wanadamu kwa Mungu kwa hiyo sifa zao zilikuwa

1.       Walichaguliwa kutoka miongoni mwa wanadamu ili kuwawakilisha wanadamu

2.       Walichaguliwa na Mungu mwenyewe

3.       Walifanya kazi ya Mungu kwa niaba ya wanadamu, kwa mambo yote ya wanadamu ya kidini ili kumfikia Mungu

4.       Walikuwa na kazi ya kutoa sadaka za kuteketezwa kwaajili ya watu kwa Mungu

5.       Walikuwa na wajibu wa kuwaombea watu kwa Mungu

6.       Walikuwa na wajibu wa kuwabariki watu wa Mungu

Kwa msingi huo katika maandiko iko wazi kabisa kuwa wajibu wa kikuhani ulikuwa ni kutoa sadaka zakuteketezwa, kuwaombea watu, na kuwabariki watu kwa jina la Mungu, hata hivyo kazi zote hizi zilizokuwa zikifanywa na makuhani bado zilikuwa zinaashiria kuwa siku moja atakuja kuhani mkuu aliye bora zaidi huyu ndiye ametabiriwa kuwa kuhani mkuu kwa mfano wa Melkizedeki “Zaburi 110:1-4 “Neno la Bwana kwa Bwana wangu, Uketi mkono wangu wa kuume, Hata niwafanyapo adui zako Kuwa chini ya miguu yako.  Bwana atainyosha toka Sayuni Fimbo ya nguvu zako. Uwe na enzi kati ya adui zako; Watu wako wanajitoa kwa hiari, Siku ya uwezo wako; Kwa uzuri wa utakatifu, Tokea tumbo la asubuhi, Unao umande wa ujana wako. Bwana ameapa, Wala hataghairi, Ndiwe kuhani hata milele, Kwa mfano wa Melkizedeki.” Huyu atakuwa ni masihi ambaye hangetoka katika ukoo wa kikuhani bali katika kabila nyingine ya Yuda na ukoo wa Daudi ukuhani wake huyu utakuwa wa milele kuhani huyu vilevile ataketi katika kiti cha enzi cha Daudi milele na milele, kuhani huyu atakuwa ni mfalme na wakati huo huo kuhani kama ilivyokuwa kwa Melkizedeki, Kuhani huyu atakuwa bora zaidi ya wale wa agano la kale kutoka kabila ya walawi, Huyu ni Yesu Kristo ambaye anafanya kazi zilezile zilizokuwa zikifanywa na makuhani katika agano lililo bora zaidi Warumi 8:33-34 “Ni nani atakayewashitaki wateule wa Mungu? Mungu ndiye mwenye kuwahesabia haki. Ni nani atakayewahukumia adhabu? Kristo Yesu ndiye aliyekufa; naam, na zaidi ya hayo, amefufuka katika wafu, naye yuko mkono wa kuume wa Mungu; tena ndiye anayetuombea.” Waebrania 7:24-25 “bali yeye, kwa kuwa akaa milele, anao ukuhani wake usioondoka. Naye, kwa sababu hii, aweza kuwaokoa kabisa wao wamjiao Mungu kwa yeye; maana yu hai sikuzote ili awaombee.”  Kwa msingi huo tunaona kwamba Mungu ametupa kuhani aliyebora zaidi kutoka nje ya kabila la walawi, ambaye ni kuhani na mfalme sawa na ilivyokuwa kwa Melkizedeki

Kuhani mkuu kwa mfano wa Melkizedeki

Yesu kuwa kuhani mkuu kwa mfano wa Melkizedeki ina faida gani kwetu?  Kama wakristo? Yako mambo kadhaa ya muhimu na msingi yenye faida kwetu kwa kristo Yesu kuwa kuhani mkuu kwaajili yetu.

1.       Tunaweza kupatanishwa na Mungu

 

Kwa sababu ya kazi aliyoifanya Yesu Kristo pale msalabani kama Kuhani mkuu ametupatanisha na Mungu 2Wakoritho 5:18-20 “Lakini vyote pia vyatokana na Mungu, aliyetupatanisha sisi na nafsi yake kwa Kristo, naye alitupa huduma ya upatanisho; yaani, Mungu alikuwa ndani ya Kristo, akiupatanisha ulimwengu na nafsi yake, asiwahesabie makosa yao; naye ametia ndani yetu neno la upatanisho. Basi tu wajumbe kwa ajili ya Kristo, kana kwamba Mungu anasihi kwa vinywa vyetu; twawaomba ninyi kwa ajili ya Kristo mpatanishwe na Mungu.”

 

Wakolosai 1:19-20 “Kwa kuwa katika yeye ilipendeza utimilifu wote ukae; na kwa yeye kuvipatanisha vitu vyote na nafsi yake akiisha kufanya amani kwa damu ya msalaba wake; kwa yeye, ikiwa ni vitu vilivyo juu ya nchi, au vilivyo mbinguni.”

 

Dhambi ilisababisha uadui kati yetu na Mungu, sote tulikuwa tumefarakanishwa na Mungu lakini kupitia Kuhani mkuu kwa mfano wa Melkizedeki Neema ya Mungu imekuwa juu yetu na uadui uliokuweko kati yetu umevunjwa wote tunajua kuwa maovu huwa yanatufarikisha kwa Mungu

 

Isaya 59:1-2 “Tazama, mkono wa Bwana haukupunguka, hata usiweze kuokoa wala sikio lake si zito, hata lisiweze kusikia; lakini maovu yenu yamewafarikisha ninyi na Mungu wenu, na dhambi zenu zimeuficha uso wake msiuone, hata hataki kusikia.”

 

Lakini kupitia Mwokozi wetu Yesu Kristo hakuna uadui tena kati yetu na Mungu Warumi 5:8:-11 “Bali Mungu aonyesha pendo lake yeye mwenyewe kwetu sisi, kwa kuwa Kristo alikufa kwa ajili yetu, tulipokuwa tungali wenye dhambi. Basi zaidi sana tukiisha kuhesabiwa haki katika damu yake, tutaokolewa na ghadhabu kwa yeye. Kwa maana ikiwa tulipokuwa adui tulipatanishwa na Mungu kwa mauti ya Mwana wake; zaidi sana baada ya kupatanishwa tutaokolewa katika uzima wake. Wala si hivyo tu, ila pia twajifurahisha katika Mungu kwa Bwana wetu Yesu Kristo, ambaye kwa yeye sasa tumeupokea huo upatanisho.”            

 

2.       Tunaweza kumfikia Mungu kwa Maombi tukiwa na ujasiri

 

Sasa tunaweza kumuomba Mungu kwa ujasiri kwa sababu ya kazi kubwa ya ukuhani aliyoifanya Bwana wetu Yesu, Mwanzoni ilikuwa ngumu kumfikia Mungu na kumuomba bila kuhani mkuu kutuombea kwanza kwa kutoa sadaka ya dhambi zake na zetu ndio tupate kibali cha kumfikia Mungu na ujasiri wa mioyo yetu, Lakini kupitia ubora wa sadaka aliyoitoa kuhani huyu mkuu kwa mfano wa Melikizedeki sasa tunaweza kabisa kumuendea Mungu kwa ujasiri na kumuomba moja kwa moja ikifahamika ya kuwa tunaye mwombezi na mpatanishi mbinguni Warumi 8:33-34 “Ni nani atakayewashitaki wateule wa Mungu? Mungu ndiye mwenye kuwahesabia haki. Ni nani atakayewahukumia adhabu? Kristo Yesu ndiye aliyekufa; naam, na zaidi ya hayo, amefufuka katika wafu, naye yuko mkono wa kuume wa Mungu; tena ndiye anayetuombea.” Waebrania 7:24-25 “bali yeye, kwa kuwa akaa milele, anao ukuhani wake usioondoka. Naye, kwa sababu hii, aweza kuwaokoa kabisa wao wamjiao Mungu kwa yeye; maana yu hai sikuzote ili awaombee.” Tunaoujasiri ya kuwa Mungu anasikia maombi yetu na kuwa atatujibu sawa na mapenzi yake kwanini kwa sababu mwanzoni ilikuwa ngumu Yohana 9:31 “Twajua ya kuwa Mungu hawasikii wenye dhambi; bali mtu akiwa ni mcha Mungu, na kuyafanya mapenzi yake, humsikia huyo.”

 

3.       Tunapata amani nafsini mwetu

 

Jambo lingine bora zuri na la amani ni kuwa tunapata amani katika dhamiri zetu hii pia ni kutokana na kazi kubwa aliyoifanya Bwana wetu Yesu Kristo pale Msalabani, Waebrania 4:14-16 “Basi, iwapo tunaye kuhani mkuu aliyeingia katika mbingu, Yesu, Mwana wa Mungu, na tuyashike sana maungamo yetu. Kwa kuwa hamna kuhani mkuu asiyeweza kuchukuana nasi katika mambo yetu ya udhaifu; bali yeye alijaribiwa sawasawa na sisi katika mambo yote, bila kufanya dhambi.  Basi na tukikaribie kiti cha neema kwa ujasiri, ili tupewe rehema, na kupata neema ya kutusaidia wakati wa mahitaji.”

4.       Sisi sasa ni makuhani pia.

 

Moja ya faida kubwa tunayoipata katika ukuhani wa Yesu Kristo, ni pamoja na sisi kuwa tunaushiriki huo ukuhani hivyo kila aaminiye ni kuhani 1Petro 2:9-10 “       Bali ninyi ni mzao mteule, ukuhani wa kifalme, taifa takatifu, watu wa milki ya Mungu, mpate kuzitangaza fadhili zake yeye aliyewaita mtoke gizani mkaingie katika nuru yake ya ajabu; ninyi mliokuwa kwanza si taifa, bali sasa ni taifa la Mungu; mliokuwa hamkupata rehema, bali sasa mmepata rehema.”

 

Ufunuo 1:4-6  Yohana, kwa yale makanisa saba yaliyoko Asia; Neema na iwe kwenu na amani, zitokazo kwake yeye aliyeko na aliyekuwako na atakayekuja; na zitokazo kwa roho saba walioko mbele ya kiti chake cha enzi; tena zitokazo kwa Yesu Kristo, shahidi aliye mwaminifu, mzaliwa wa kwanza wa waliokufa, na mkuu wa wafalme wa dunia. Yeye atupendaye na kutuosha dhambi zetu katika damu yake, na kutufanya kuwa ufalme, na makuhani kwa Mungu, naye ni Baba yake; utukufu na ukuu una Yeye hata milele na milele. Amina.”

 

Raha ya aina yake kuwa na kuhani mkuu wa kipekee mwenye Baraka zetu zote za kimwili na kiroho!

 

Rev. Innocent Kamote.

 

Mkuu wa wajenzi mwenye Hekima!

Jiwe la Kukwaza Katika Sayuni !


1Petro 2:6-8 “Kwa kuwa imeandikwa katika maandiko Tazama, naweka katika Sayuni jiwe kuu la pembeni, teule, lenye heshima, Na kila amwaminiye hatatahayarika.  Basi, heshima hii ni kwenu ninyi mnaoamini. Bali kwao wasioamini, Jiwe walilolikataa waashi, Limekuwa jiwe kuu la pembeni. Tena, Jiwe la kujikwaza mguu, na mwamba wa kuangusha, Kwa maana hujikwaza kwa neno lile,wasiliamini,nao waliwekwa kusudi wapate hayo.”


Utangulizi:

Ni muhimu kufahamu kuwa ni kwanini mtume Petro anamtaja Yesu Kristo kama jiwe la kukwaza? (Stumbling block) Hili linaweza kuwa jambo lenye kushangaza sana, kwa sababu kwa lugha rahisi hauwezi kudhani kuwa Mungu angeweza kukusudia Kristo Yesu awe jiwe la Kukwaza pia, Katika hali ya kawaida tunapomuelezea Yesu Kristo kama jiwe la Pembeni na lenye heshima inaweza kueleweka vema zaidi, lakini hata hivyo kama tutaelewa kile kinacho maanishwa katika maandiko tunaweza kutoka tukiwa na amani ya kutosha sana kumuhusu Yesu Kristo na sisi tuliomuamini. Tutajifunza somo hili kwa kuzinagatia vipengele vifuatavyo vikuu viwili vifuatavyo:-

·         Maana ya jiwe la kukwaza.

·         Jiwe la kukwaza katika Sayuni. 

Maana ya jiwe la kukwaza.

Kibiblia neno jiwe la kukwaza au kukwaza maana yake ni kukosesha kwa hila kwa kiingereza ni Stumbling Block yaani ukwazo, au makwazo ambalo kwa kiibrania husomeka kama neno Miksol na kwa kiyunani ni Skandalon ambalo maana yake ni kukosesha au kutegea mtu ili aanguke na kupata madhara au jambo lolote linaloweza kufanyika na kumfanya mtu afanye dhambi au apatikane na madhara na kuhukumiwa sawa na kumuwekea mtu mtego ili aingie hatiani 

Zaburi 140:4-5 “Ee Bwana, unilinde na mikono ya mtu asiye haki; Unihifadhi na mtu wa jeuri; Waliowaza kuzipotosha hatua zangu. Wenye kiburi wamenifichia mtego na kamba; Wametandika wavu kando ya njia; Wameniwekea matanzi.”

Jambo hili kimaandiko sio jambo jema na Katika lugha ya kinabii kukosesha mtu au kumkwaza mtu kulihesabika kuwa ni tukio baya, hasa linapofanyika kwa mtu asiye na hatia, Mungu aliwaagiza makuhani kutokuweka kwazo kwa mtu asiye na ufahamu au asiyeona (kipofu) kwani kufanya hivyo lilionekana kuwa jambo baya na la kikatili sana  

Walawi 19: 14 “Usimlaani kiziwi, wala usitie kwazo mbele ya kipofu, bali umche Mungu wako; Mimi ndimi BWANA.”

Kimsingi maandiko haya yalikuwa na maana ya kutokusababisha makwazo kwa watu wanaohitaji kuelekezwa au kufahamishwa, kwa hiyo kimsingi maonyo haya yanawahusu walimu wa neno la Mungu kwamba wasitumie ufahamu wao kuwapotosha watu kwa hila kwa kufanya hivyo kungeleta hukumu iliyokubwa sana au ya kutisha ona

 Mathayo 18:6 “bali atakayemkosesha mmojawapo wa wadogo hawa waniaminio, yamfaa afungiwe shingoni jiwe kubwa la kusagia, na kutoswa katika kilindi cha bahari.

Unaweza kuona maandiko yanatangaza hukumu kubwa sana kwa mtu atakayekosesha wengine au kwa lugha nyingine anayesababisha makwazo au kwa lugha nyingine kufundisha watu uongo au kumtia mwenye haki hatiani

Yakobo 3:1-2 “Ndugu zangu, msiwe waalimu wengi, mkijua ya kuwa mtapata hukumu kubwa zaidi. Maana twajikwaa sisi sote pia katika mambo mengi. Mtu asiyejikwaa katika kunena, huyo ni mtu mkamilifu, awezaye kuuzuia na mwili wake wote kama kwa lijamu.”  

Kwa msingi huo unaweza kupata picha ya wazi kuwa kukosesha au kukwaza kamwe kibiblia halikuweza kuhesabiwa kuwa  la jambo zuri bali ni tukio baya na lililoambatana na maonyo makali dhidi ya wale wote wanaosababisha makwazo ya aina yoyote ile :-

Luka 17:1-2 “Akawaambia wanafunzi wake, Makwazo hayana budi kuja, lakini ole wake mtu yule ambaye yaja kwa sababu yake! Ingemfaa zaidi mtu huyo jiwe la kusagia lifungwe shingoni mwake, akatupwe baharini, kuliko kumkosesha mmojawapo wa wadogo hawa.  

Sasa ni katika namna ya kushangaza sana unaweza kustaajabu kuona kuwa ujio wa Masihi Bwana wetu Yesu Kristo unatajwa vilevile kuambatana na Heshima kwa wale watakaomwamini lakini vilevile na kukwaza  kwa wale watakaomkataa au kutokumuelewa na kutokumuamini hii maana yake ni nini hilo sasa linatuleta kutafakari kipengele kinachofuata kama ifuatavyo:-         

Jiwe la kukwaza katika sayuni

Ni muhimu kufahamu kuwa kuja kwa Yesu Kristo duniani, kulitabiriwa na manabii na kuwekwa wazi kuwa Yesu angekuja kwa makusudi makuu mawili, yaani kuokoa wengi  na kuwapa heshima kubwa lakini vilevile kukwaza wengi hasa wale wasiomuamini au wasiomuelewa na kumkubali na kusababisha hukumu kubwa sana kwao, 

Yohana 3:16 -18 “Kwa maana jinsi hii Mungu aliupenda ulimwengu, hata akamtoa Mwanawe pekee, ili kila mtu amwaminiye asipotee, bali awe na uzima wa milele. Maana Mungu hakumtuma Mwana ulimwenguni ili auhukumu ulimwengu, bali ulimwengu uokolewe katika yeye. Amwaminiye yeye hahukumiwi; asiyeamini amekwisha kuhukumiwa; kwa sababu hakuliamini jina la Mwana pekee wa Mungu.”

Kwa msingi huo ujio wa Yesu Kristo una maswala makubwa mawili ya msingi kwa wanaomuamini na kwa wasiomuamini, wanaomuamini hawatatahayarika lakini kwa wale wasiomuamini watapata hukumu watakutana na mambo magumu sana sawa na alivyotabiri nabii isaya ona.  

Isaya 28:16 “kwa ajili ya hayo Bwana, MUNGU, asema hivi, Tazama, naweka jiwe katika Sayuni, liwe msingi, jiwe lililojaribiwa, jiwe la pembeni lenye thamani, msingi ulio imara; yeye aaminiye hatafanya haraka.”

Swala hili lilielezwa mapema katika maandiko lakini vilevile nabii mwingine alimuelezea Mariamu mama yake Yesu waziwazi mara baada ya kuzaliwa na walipokuwa wamempeleka kijana Yesu Hekaluni kwa kubarikiwa ona katika

Luka 2: 25-34 “Na tazama, pale Yerusalemu palikuwa na mtu, jina lake Simeoni, naye ni mtu mwenye haki, mcha Mungu, akiitarajia faraja ya Israeli; na Roho Mtakatifu alikuwa juu yake. Naye alikuwa ameonywa na Roho Mtakatifu ya kwamba hataona mauti kabla ya kumwona Kristo wa Bwana. Basi akaja hekaluni ameongozwa na Roho; na wale wazazi walipomleta mtoto Yesu ndani, ili wamfanyie kama ilivyokuwa desturi ya sheria, yeye mwenyewe alimpokea mikononi mwake, akamshukuru Mungu, akisema, Sasa, Bwana, wamruhusu mtumishi wako, Kwa amani, kama ulivyosema; Kwa kuwa macho yangu yameuona wokovu wako, Uliouweka tayari machoni pa watu wote; Nuru ya kuwa mwangaza wa Mataifa, Na kuwa utukufu wa watu wako Israeli.  Na babaye na mamaye walikuwa wakiyastaajabia hayo yaliyonenwa juu yake. Simeoni akawabariki, akamwambia Mariamu mama yake, Tazama, huyu amewekwa kwa kuanguka na kuinuka wengi walio katika Israeli, na kuwa ishara itakayonenewa.”

Kuna maneno kadhaa ambayo watafasiri wa biblia ya Kiswahili waliyachanganya au kuyanukuu vibaya hasa katika mstari wa 34 hapo ambao katika biblia ya Kiswahili Union Version unasomeka hivi Simeoni akawabariki, akamwambia Mariamu mama yake, Tazama, huyu amewekwa kwa kuanguka na kuinuka wengi walio katika Israeli, na kuwa ishara itakayonenewa.” Mstari huo katika biblia ya  kiingereza  ya NIV yaani New International version unasomeka hiviThen Simeon blessed them and said to Mary, his mother: This child is destined to cause the Falling and rising of many in Israel, and to be a sign that will be spoken againstkwa hiyo kwa tafasiri yangu mimi kifungu hiki kilitakiwa kusomeka Simeoni akawabarikia na kumwambia Mariam, mama yake, Mtoto huyu hatima yake itasababisha kuanguka (Kujikwaa) na kuinuka (kuokolewa) kwa wengi katika Israel  na kuwa Ishara itakayonenwa kinyume  unaona Kwa msingi huo Petro anamuelezea Yesu katika pande hizo mbili ya kuwa ni jiwe zuri sana la thamani na heshima kwa wale walimuamini lakini vilevile ni jiwe la kukwaza kwa wale waliomkataa na wasiomuelewa, au waliompuuzia, Wakati wote Yesu alipokuwa duniani na kufanya kazi yake  makundi mawili yalitokea wale waliomuamini na wale wasiomuamini na wale wasiomuamini Kristo wamepata hasara kubwa sana Yohana 6:54-62 Petro anatoa ushauri kwa waamini waendelee kumfuata Yesu kwa sababu yeye ni jiwe lililo hai, ni jiwe teule, ni jiwe lenye heshima na kwa kufanya hivyo hakuna mtu atakayetahayari au atakayeaibika kwa kumtegemea Yesu. 

1Petro 2:4-9 “Mmwendee yeye, jiwe lililo hai, lililokataliwa na wanadamu, bali kwa Mungu ni teule, lenye heshima. Ninyi nanyi, kama mawe yaliyo hai, mmejengwa mwe nyumba ya Roho, ukuhani mtakatifu, mtoe dhabihu za roho, zinazokubaliwa na Mungu, kwa njia ya Yesu Kristo. Kwa kuwa imeandikwa katika maandiko Tazama, naweka katika Sayuni jiwe kuu la pembeni, teule, lenye heshima, Na kila amwaminiye hatatahayarika. Basi, heshima hii ni kwenu ninyi mnaoamini. Bali kwao wasioamini, Jiwe walilolikataa waashi, Limekuwa jiwe kuu la pembeni.Tena, Jiwe la kujikwaza mguu, na mwamba wa kuangusha, Kwa maana hujikwaza kwa neno lile,wasiliamini,nao waliwekwa kusudi wapate hayo. Bali ninyi ni mzao mteule, ukuhani wa kifalme, taifa takatifu, watu wa milki ya Mungu, mpate kuzitangaza fadhili zake yeye aliyewaita mtoke gizani mkaingie katika nuru yake ya ajabu;    
    

Petro anakazia katika ujumbe wake sawa na neno la Mungu kwa vinywa vya manabii ya kuwa tumchague Yesu, yeye ni jiwe lenye heshima ni teule limendaliwa na Mungu baba kwaajili ya ukombozi wetu na kwamba ni fahari kumuamini Yesu na kumkubali na kuwa yeye hatatukataa na kuwa hatutatahayari, yesu hatamuangusha mtu awaye yote anayemtumaini na kumwendea yeye wakati wowote hata tuwapo majaribuni, hatatuangusha kwa hiyo ukimuamini Yesu na kumtegemea katika maisha yako kutoboa katika jambo lolote kuko nje nje lakini ukimpuuzia Yesu aibu na makwazo na hukumu zinakungoja ona katika maandiko:- 

Warumi 9:33 “kama ilivyoandikwa, Tazama, naweka katika Sayuni jiwe likwazalo, na mwamba uangushao; Na kila amwaminiye hatatahayarika.”  

Kumwamini Yesu kunalipa na kuliwapa faida kubwa wale waliomsadiki, lakini wale wanaojifanya wana hekima na akili na wanaomtambua Yesu kama mtu wa kawaida watajikwaa, watu hawajikwai kwa Yesu tu wanajikwaa hata kwa neno lake na kukataa ujumbe wake hata leo, Yesu hatambuliki kwa historia ya kibinadamu tu na hekima ya kibinadamu tu huwezi kumtambua Yesu kwa hisia tu, au kwa ujuzi wako binafsi, wako watu waliojikwaa kwa sababu walimuona Yesu kuwa ni wa kawaida tu wakitimia akili zao na hekima ya kibinadamu watu wengi wataingia dhambini na hatimaye kuingia mtoni kwa sababu ya kutumia fahamu zao katika maswala ya kiungu, wako watu wenye dharau kubwa sana kuhusu Mungu, na mambo ya Mungu huonekana kama ya kipumbavu kwao, na wengine hulichukulia neno la Mungu kwa mazoea tu  jambo hili litawagharimu gharama kubwa sana kwa sababu watajikwaa na ukijikwaa hukumu itakupasa 

Marko 6:1-3 “Akatoka huko, akafika mpaka nchi ya kwao; wanafunzi wake wakamfuata. Na ilipokuwa sabato, alianza kufundisha katika sinagogi; wengi waliposikia wakashangaa, wakisema, Huyu ameyapata wapi haya? Na, Ni hekima gani hii aliyopewa huyu? Na, Ni nini miujiza hii mikubwa inayotendeka kwa mikono yake? Huyu si yule seremala, mwana wa Mariamu, na ndugu yao Yakobo, na Yose, na Yuda, na Simoni? Na maumbu yake hawapo hapa petu? Wakajikwaa kwake.” 

Hatuwezi kumtambua Yesu kwa akili za kawaida na ujuzi wa kawaida Yesu alikuja ili wanyenyeevu watu waliovunjika moyo waweze kumkubali na watu wenye kiburi waweze kukataliwa Yesu ataendelea kuwa jiwe la kukwaza kwa watu wote wanaojidhani kuwa wana hekima ya mwilini na watu wote wenye kiburi na wale wanaojihesabia haki na ndio maana Yesu alipokuja duniani Mafarisayo ambao  walifikiriwa kuwa ndio wenye Haki waliumbuliwa na kujulikana kama wanafiki, wale waliokuwa wakiitumainia haki yao wenyewe waliumbuka na kujiona kuwa sio kitu kila mtu anayejitumainia na kujiamini mwenyewe Yesu kama jiwe la kukwaza litawasaga tikitiki, watu wasio na akili huitegemea akili yao wenyewe, lakini Yesu ameifanya hekima ya dunia hii kuwa ni upuuzi na kuifanya kuwa si kitu ni kupitia kumwamini Yesu tu tunaweza kuokolewa na kuhesabiwa haki kutoka kwa Mungu, kila anayemuami Yeye hatatahayari wala hatakwazika lakini kila anayejitumainia atakwazika na kukengeuka na kuingia katika hukumu ya Mungu. Mungu hawezi kueleweka kwa hekima ya kibinadamu, wengi waliokosa Baraka za Mungu ni wale waliopuuzia neno la Mungu na kuona kama Yesu hana maana lakini wale wanaomkubali wanazijua nguvu zake na uwezo wake 

1Wakoritho 1:18-19 “Kwa sababu neno la msalaba kwao wanaopotea ni upuzi, bali kwetu sisi tunaookolewa ni nguvu ya Mungu. Kwa kuwa imeandikwa, Nitaiharibu hekima yao wenye hekima, Na akili zao wenye akili nitazikataa.”   
              

Rev. Innocent Samuel Kamote.

Mkuu wa wajenzi mwenye Hekima