Jumanne, 28 Machi 2023

Mungu Katikati ya shida zako !


Zaburi 138:6-8 “Ingawa Bwana yuko juu, amwona mnyenyekevu, Naye amjua mwenye kujivuna tokea mbali. Nijapokwenda kati ya shida utanihuisha, Utanyosha mkono juu ya hasira ya adui zangu, Na mkono wako wa kuume utaniokoa. Bwana atanitimilizia mambo yangu; Ee Bwana, fadhili zako ni za milele; Usiziache kazi za mikono yako.”



Utangulizi:

Duniani ni mahali ambapo pana changamoto za aina mbalimbali ambazo kila mwanadamu aliyezaliwa na mwanamke atakutana nazo, wakati mwingine tutakutana na hali ngumu sana ama upinzani mzito sana, au magonjwa makubwa ya kusumbua au kuwa na ndoto kubwa  ambazo tunatafuta namna ya kuzitimiza, na changamoto nyinginezo nyingi, na wakati mwingine hali Fulani za kukatisha tamaa na kuvunja moyo na ama wakati mwingine ukiwa katika vita kali sana, katika ndoa, katika kazi, katika masomo, katika biashara, katika mashamba, katika mifugo na katika mahusiano taabu hizi zote Yesu Kristo anazifahamu na anajua ya kuwa tunazipitia na alitutaka tujipe moyo kwa sababu yeye amezishinda kwaajili yetu. 

Yohana 16:33 “Hayo nimewaambieni mpate kuwa na amani ndani yangu. Ulimwenguni mnayo dhiki; lakini jipeni moyo; mimi nimeushinda ulimwengu.” 

Yesu anazungumza maneno haya kwa sababu anatambua wazi kuwa wakati mwingine tunaweza kujiona kama tuna mapungufu Fulani nani kama hatutoshi wala hatustahili hata kufanyiwa muujiza, lakini ni muhimu sana kukumbuka ya kuwa Mungu yuko pamoja nasi yeye anaitwa Emmanuel yaani Mungu pamoja nasi na wakati tunapopitia kila aina ya changamoto na mambo yoyote yanayotukabili yeye yuko pamoja nasi, alikuwa pamoja na Yesu Kristo katika mateso yake na alihakikisha anamfufua, na hakumuacha kaburini, wakati Daudi anakabiliana na jitu kubwa kuliko uwezo wake Mungu alikuwa pamoja naye, wakati Paulo na Sila wakiwa gerezani ni yeye aliyafungua milango ya gereza, wakati Danieli anatupwa katika tundu la Simba ni yeye aliyekuweko kufunga makanwa ya simba, na wakati Shadrak, Meshak na Abednego wakitupwa kwenye tanuri la moto mkali ni yeye ndiye aliyejiunga nao wasiunguzwe jambo kubwa la msingi ni kukumbuka tu ya kuwa Mungu yuko kati kati ya shida zako. 

Zaburi 138:6-8 “Ingawa Bwana yuko juu, amwona mnyenyekevu, Naye amjua mwenye kujivuna tokea mbali. Nijapokwenda kati ya shida utanihuisha, Utanyosha mkono juu ya hasira ya adui zangu, Na mkono wako wa kuume utaniokoa. Bwana atanitimilizia mambo yangu; Ee Bwana, fadhili zako ni za milele; Usiziache kazi za mikono yako.” 

Katika mistari hii ya msingi hususani mstari ule wa saba yaani Zaburi ya 138:7 “Nijapokwenda kati ya shida utanihuisha, Utanyosha mkono juu ya hasira ya adui zangu, Na mkono wako wa kuume utaniokoa.  Mungu nanatufundisha kupitia mtumishi wakeMwandishi wa zaburi hii ya kuwa yeye huwa katikakati ya shida zetu mstari huu katika lugha ya kiingereza Biblia ya NIV husomeka hiviThough I walk in the midst of trouble, you preserve my life you stretch out your hand against the anger of my foes with your hand you save meambapo katika tafasiri yangu naweza kusema Mstari huu unasema hivi NINAPOPITA KATIKATI YA TAABU/SHIDA UNANYOOSHA MKONO WAKO KUNIOKOA NA HASIRA ZA ADUI ZANGU, Yaani maana yake katikati ya shida Mungu anakuwepo, na anatoa msaada kwaajili ya utukufu wake hii maana yake ni nini ? sio kila wakati Mungu atakutoa nje ya shida lakini wakati mwingine atakuacha uingie katika shida na changamoto mbalimbali kisha ataweka mkono wake kwaajili ya utukufu wake, kwa sababu hiyo jambo kubwa la Msingi na la kukumbuka ni kuwa Bwana yuko pamoja nawe bila kujali hali unayoipitia, kuokolewa katika shida sio jambo la Msingi sana kama Mungu kuwa pamoja nawe, Mungu kuwa pamoja nawe hilo ndio jambo kubwa na la msingi, 

Isaya 43:1-2 “Lakini sasa, Bwana aliyekuhuluku, Ee Yakobo, yeye aliyekuumba, Ee Israeli, asema hivi, Usiogope, maana nimekukomboa; nimekuita kwa jina lako, wewe u wangu. Upitapo katika maji mengi nitakuwa pamoja nawe; na katika mito, haitakugharikisha; uendapo katika moto, hutateketea; wala mwali wa moto hautakuunguza.” 

Unaona haijalishi kuna dhuruba kiasi gani kama Mungu yuko pamoja nawe hakuna kitakachoshindikana kwaajili ya utukufu wake, Mungu atatokeza muujiza kwa sababu yumo katikati ya shida yako pamoja nawe 

Kumbuka kuwa 

1.       Wakati Suleiman anaanza kutawala alikuwa na hofu kuwa anawezaje kuongoza taifa kubwa na watu wengi kama wale, baba yake alikuwa mtu wa vita na mtu aliyemtegemea Mungu, hivyo Mungu alimsaidia Suleimani kuwa na hekima ya namna ya kuingia na kutoka na mambo yakawa shwari 

2.       Mungu hakumuwacha Yesu asisulubiwe lakini alimfufua siku ya tatu, hakumwacha mtakatifu wake aonje uharibifu

3.       Mungu hakumwacha Nyangumi asimmeze Yona na badala yake alimsababisha nyangumi amtapike Yona siku ya tatu

4.       Mungu hakumuacha Daniel asiingizwe kwenye tundu la Simba badala yake aliyafunga makanwa ya simba

5.       Mungu hakuwaacha Shadrak na Meshak na Abednego wasitupwe katika tanuru la Moto lakini badala yake alijiunga nao katikati ya Moto ili usiwateteze

6.       Mungu hakuwaacha Paulo na Silas wasipigwe na kutupwa gerezani lakini badala yake aliwaacha wakafungwa gerezani na baadaye akayafungua malango ya magereza na vifungo vyake   

Changamoto kubwa katika maisha yetu sio kutokupitia changamoto bali ni kumuomba Mungu awe pamoja nasi hili ndilo jambo la Msingi Yesu aliahidi ya kuwa atakuwa pamoja nasi hata ukamilifu wa dahari, na alihahidi kuwa tunapokutanika wawili au watatu kwa ajili ya jina lake atakuwa pamoja nasi, Hakuna jambo la msingi duniani kama kuwa na Mungu, Muulize jirani yako una Mungu ukiwa na Mungu una kila kitu!, Changamoto yako sio kubwa kuliko Mungu tunayemtumikia na kumuabudu, Bwana ampoe neema kila mmoja wetu kuwa na Mungu wakati tunapopita katika siku za kujaribiwa kwetu katika jina la Yesu Kristo amen! 

Na Rev. Innocent Kamote

Mkuu wa wajenzi mwenye Hekima!



Alhamisi, 23 Machi 2023

Chanda cha Mungu !


Kutoka 8: 16 -19 “BWANA akamwambia Musa, Mwambie Haruni, Nyosha fimbo yako, ukayapige mavumbi ya nchi, ili kwamba yawe chawa katika nchi yote ya Misri. Nao wakafanya; Haruni akaunyosha mkono wake na fimbo yake, na kuyapiga mavumbi ya nchi, nayo yakawa chawa juu ya wanadamu na juu ya wanyama; mavumbi yote ya nchi yakawa ni chawa katika nchi yote ya Misri. Hao waganga nao wakafanya mfano wa hayo kwa uganga wao, ili kwamba walete chawa, lakini wasiweze; nako kulikuwa na chawa juu ya wanadamu, na juu ya wanyama. Ndipo wale waganga wakamwambia Farao, Jambo hili ni chanda cha Mungu; na moyo wake Farao ukawa mgumu asiwasikize; vile vile kama BWANA alivyonena.”




Utangulizi:

Neno Chanda cha Mungu limejitokeza au kutajwa katika Biblia ya Kiebrania kama neno “etsba” kimatamshi “ets-bah” na kutajwa katika Biblia ya kiingereza ya King James Version mara 32  na kwa lugha ya kiyunani ni “Daktulos” kimatamshi ni Dak-too-los  ambalo Katika Biblia ya kiingereza ya King James Version limetajwa mara 8, maneno yote hayo katika lugha ya kiibrania na kiyunani yanamaanisha kidole cha Mungu, Neno ambalo kinabii linahusiana na Utendaji wa Roho Mtakatifu, hata hivyo Pamoja na neno hilo kutajwa mara kadhaa, limeonekana kwa uwazi katika matukio kadhaa likitumika kwa namna kali zaidi ya maeneo mengine.

·         Kidole cha Mungu wakati wa Farao.

·         Kidole cha Mungu Katika mlima wa Sinai.

·         Kidole cha Mungu wakati wa Beltshaza.

·         Kidole cha Mungu na wakati wa Huduma ya Yesu.

Kidole cha Mungu wakati wa Farao!

Neno kidole cha Mungu linajitokeza kwa mara ya kwanza katika lugha za kinabii, kutokana na uandishi wa Musa katika kitabu cha kutoka mara baada ya Musa na Haruni kuamuriwa na Mungu kuachilia pigo la tatu, Mapigo haya yalikuwa ni amri ya Mungu ili kumlazimisha Farao kuwaachia wana wa Israel waende zao kwa sababu walikaa katika inchi ya Misri na katika hali ya utumwa kwa zaidi ya miaka 400, Mungu alimuelekeza Musa kumuamuru Haruni kunyoosha fimbo yake ili kuyapiga mavumbi ya nchi yapate kuwa chawa katika inchi yote ya Misri

Kutoka 8:16-17BWANA akamwambia Musa, Mwambie Haruni, Nyosha fimbo yako, ukayapige mavumbi ya nchi, ili kwamba yawe chawa katika nchi yote ya Misri. Nao wakafanya; Haruni akaunyosha mkono wake na fimbo yake, na kuyapiga mavumbi ya nchi, nayo yakawa chawa juu ya wanadamu na juu ya wanyama; mavumbi yote ya nchi yakawa ni chawa katika nchi yote ya Misri.”

Kwa kawaida kila Muujiza ambao Musa na Haruni waliufanya kwa jina la Mungu, utaweza kuona wachawi wa kimisri nao waliigiza hasa kwa miujiza ya mwanzoni walipojaribu kuuigiza muujiza huu kwa uchawi wao na kushindwa ndipo walipotamka wenyewe kwa midomo yao kumueleza Farao kuwa hiki ni chanda cha Mungu,

Kutoka 8:18-19 “Hao waganga nao wakafanya mfano wa hayo kwa uganga wao, ili kwamba walete chawa, lakini wasiweze; nako kulikuwa na chawa juu ya wanadamu, na juu ya wanyama. Ndipo wale waganga wakamwambia Farao, Jambo hili ni CHANDA CHA MUNGU; na moyo wake Farao ukawa mgumu asiwasikize; vile vile kama BWANA alivyonena.”  Hapo ndipo tunapouona uweza wa Mungu katika kutenda miujiza ya kupita kawaida dhidi ya miujiza ya kichawi na ya kimazingaombwe, Mungu ana uwezo mkubwa sana, anapukusudia kutukomboa katika utumwa wa anina yoyote ile ni lazima tumuitie yeye kwa uweza wa Roho wake Mtakatifu ambaye ndiye chanda cha Mungu atatutoa katika mikandamizo ya aina yoyote ile                            

Kidole cha Mungu Katika mlima wa Sinai.

Eneo lingine ambapo tunaona maandiko yakitaja chanda cha Mungu ni katika Mlima wa Sinai wakati Mungu alipokuwa anataka kumpa Musa Amri na sharia zake ili awafundishe watu wake, wakati Amri Kumi za Msingi zilipokuwa zinaandikwa tunaelezwa kuwa amri hizo ziliandikwa kwa kidole cha Mungu yaani Chanda cha Mungu

Kutoka 31:18 “Hapo BWANA alipokuwa amekwisha zungumza na Musa katika mlima wa Sinai, akampa hizo mbao mbili za ushuhuda, mbao mbili za mawe, zilizoandikwa kwa chanda cha Mungu.”

Musa analikumbuka tukio hilo la amri na sharia za Mungu kuandikwa kwa kidole chake wakati alipokuwa anawaandikia kitabu kingine cha kumbukumbu la Torati ona katika

Kumbukumbu la Torati 9:9 -10 “Na hapo nilipokwea mlimani kwenda kuzipokea mbao za mawe, nazo ni mbao za agano Bwana alilofanya nanyi, ndipo nikakaa mle mlimani siku arobaini usiku na mchana; sikula chakula wala kunywa maji. Bwana akanipa zile mbao mbili za mawe zimeandikwa kwa kidole cha Mungu; na juu yake yameandikwa maneno mfano wa yote aliyosema nanyi Bwana mle mlimani toka kati ya moto siku ya mkutano.”  

Haikuwa lazima kuwa labda Mungu aliandika ka ma wanadamu waandikavyo kwa kuwa Mungu ni Roho lakini haipingiki kuwa uwezo wake wa utendaji ROHO MTAKATIFU alisababisha kwa muujiza mkubwa sharia zake za msingi kuwepo katika mawe yale, ni ukweli usiopingika kuwa kama Roho Mtakatifu aliweza kuziandika sharia za Mungu katika mawe hashindwi kuziandika sharia zake katika mioyo yetu neno la Mungu linaeleza wazi kuwa uko wakati ambapo Mungu ataziandika sheria zake katika mioyo yetu  

2 Wakoritho 3:2-3  Ninyi ndinyi barua yetu, iliyoandikwa mioyoni mwetu, inajulikana na kusomwa na watu wote; mnadhihirishwa kwamba mmekuwa barua ya Kristo tuliyoikatibu, iliyoandikwa si kwa wino, bali kwa Roho wa Mungu aliye hai; si katika vibao vya mawe, ila katika vibao ambavyo ni mioyo ya nyama.”  

Unaona Roho Mtakatifu yaani utendaji wa Mungu ulioandika sharia kwa kidole cha Moto katika mlima wa Sinai yu aweza kuandika sheria zake na kuweka mwako wa moto katika mioyo yetu ili tumtii Mungu, tunaweza kusoma mapenzi ya Mungu leo kutoka Moyoni kwa kuelekezwa na kufundishwa na Roho Mtakatifu

1Yohana 3:21-24 “Wapenzi, mioyo yetu isipotuhukumu, tuna ujasiri kwa Mungu; na lo lote tuombalo, twalipokea kwake, kwa kuwa twazishika amri zake, na kuyatenda yapendezayo machoni pake. Na hii ndiyo amri yake, kwamba tuliamini jina la Mwana wake Yesu Kristo, na kupendana sisi kwa sisi, kama alivyotupa amri. Naye azishikaye amri zake hukaa ndani yake yeye naye ndani yake. Na katika hili tunajua ya kuwa anakaa ndani yetu, kwa huyo Roho aliyetupa.”

 Utendaji wa Mungu ndani yetu unaweza kuihuisha sharia ya Mungu ndani yetu na kutugeuza kuwa mfano wa kuigwa kwa kila mtu duniani, hata kama ulimwengu unaweza kuwa umeharibika kwa kiwango gani Roho Mtakatifu ndani yetu atatuongoza na kutuhifadhi na kuionya mioyo yetu na kutuelekeza katika sharia ya Mungu wetu sharia ya kifalme sharia ya Roho wa Uzima kwa sababu hiyo sisi sasa hatuongozwi na sharia ile ya kimwili iletayo mauti bali twaongozwa na sharia ya Roho wa Uzima ulio katika Kristo Yesu.

Warumi 8:1-4Sasa, basi, hakuna hukumu ya adhabu juu yao walio katika Kristo Yesu. Kwa sababu sheria ya Roho wa uzima ule ulio katika Kristo Yesu imeniacha huru, mbali na sheria ya dhambi na mauti. Maana yale yasiyowezekana kwa sheria, kwa vile ilivyokuwa dhaifu kwa sababu ya mwili, Mungu, kwa kumtuma Mwanawe mwenyewe katika mfano wa mwili ulio wa dhambi, na kwa sababu ya dhambi, aliihukumu dhambi katika mwili; ili maagizo ya torati yatimizwe ndani yetu sisi, tusioenenda kwa kufuata mambo ya mwili, bali mambo ya roho.”      

Kidole cha Mungu wakati wa Beltshaza.

Eneo lingine ambapo tunauona utendaji wa Mungu kama Kidole chake ni wakati wa kipindi cha utawala wa mfalme Mpumbavu aliyeitwa Belshaza mfalme huyu hakujua ya kuwa Mungu ndiye anayeweka watu madarakani, yeye aliamuru vyombo vilivyokuwa vimetekwa kutoka Hekalu lililokuwako Yerusalem, na baba yake Mfalme mkuu Nebukadreza ambaye baadaye alimuheshimu sana Mungu wa Israel, lakini Belshaza yeye alikuwa na dharau hakuthamini vyombo vile vya Hekaluni ambavyo kimsingi vilikuwa vimewekwa wakfu, chombo kinapokuwa kimewekwa Wakfu maana yake Roho wa Mungu anakuwa amevitenga na kuviheshimu lakini Beslshaza badala yake yeye aliamua kuvidhalilisha kwa kuvinywea pombe ona katika

Daniel 5:1-4 “Belshaza, mfalme, aliwafanyia wakuu wake elfu karamu kubwa akanywa divai mbele ya elfu hao. Belshaza, alipokuwa akionja ile divai, akaamuru wavilete vile vyombo vya dhahabu na fedha, ambavyo baba yake, Nebukadreza, alivitoa katika hekalu lililokuwako Yerusalemu; ili kwamba mfalme, na wakuu wake, na wake zake, na masuria wake, wapate kuvinywea. Basi wakavileta vile vyombo vya dhahabu, vilivyotolewa katika hekalu la nyumba ya Mungu lililokuwako Yerusalemu; na mfalme na wakuu wake, na wake zake, na masuria wake, wakavinywea. Wakanywa divai, wakaisifu miungu ya dhahabu, na ya fedha, na ya shaba, na ya chuma, na ya mti, na ya mawe.”

Ukweli ni wazi kuwa tukio hili lilimuuzunisha sana Mungu wa Israel, Mungu hawezi kukubali vyombo vyake alivyovoweka wakfu kwa kuvitakasa vitumike kinyume na makusudi ya Mungu aliye hai, wakati tukio hili lililpokuwa likiendelea mfalme aliona katika ukuta kiganja cha mkono kikiandika kwa vidole vya kibinadamu kumtangazia mfalme huyu hukumu yake kwa haraka ona

Daniel 5:5-6 “Saa iyo hiyo vikatokea vidole vya mkono wa mwanadamu, vikaandika katika chokaa ya ukuta wa nyumba ya enzi ya mfalme, mahali palipokikabili kinara; naye mfalme akakiona kitanga cha ule mkono ulioandika. Ndipo uso wa mfalme ukambadilika; fikira zake zikamfadhaisha; viungo vya viuno vyake vikalegea; magoti yake yakagongana.”

 Jambo hili lilikuwa jambo la kutisha sana lugha ya kibiblia hapo VIUNGO VYA VIUNO VYAKE VIKALEGEA ni lugha ya kiungwana kuwa mfalme alijinyea na kujiharishia kwa hofu, tabia mbaya aliyokuwa nayo na dhadhau yake dhidi ya mambo ya Mungu ilikuwa sasa inashughulikiwa na utendaji wa Mungu mwenyewe, vidole hivyo vya Mungu vilikuwa vimentangazia hukumu ya Mungu na hukumu yake ilikuwa ni kifo kwa sababu amevuka mpaka Daniel ambaye ndiye alikuja kuyatafasiri maneno yale alisema

Daniel 5: 22-30 “Na wewe, mwanawe, Ee Belshaza, hukujinyenyekeza moyo wako, ijapokuwa ulijua hayo yote. Bali umejiinua juu ya Bwana wa mbingu; nao wamevileta vyombo vya nyumba yake mbele yako; na wewe, na wakuu wako, na wake zako, na masuria wako, mmevinywea; nawe umeisifu miungu ya fedha na ya dhahabu na ya shaba, na ya chuma, na ya mti, na ya mawe; wasioona, wala kusikia, wala kujua neno lo lote; na Mungu yule, ambaye pumzi yako i mkononi mwake, na njia zako zote ni zake, hukumtukuza. Ndipo kile kitanga cha ule mkono kikaletwa kutoka mbele zake, na maandiko haya yameandikwa. Na maandiko yaliyoandikwa ni haya; MENE, MENE, TEKELI, NA PERESI. Na tafsiri ya maneno haya ni hii; MENE, Mungu ameuhesabu ufalme wako na kuukomesha. TEKELI, umepimwa katika mizani nawe umeonekana kuwa umepunguka. PERESI, ufalme wako umegawanyika, nao wamepewa Wamedi na Waajemi. Ndipo Belshaza akatoa amri, nao wakamvika Danieli mavazi ya rangi ya zambarau, wakatia mkufu wa dhahabu shingoni mwake, wakapiga mbiu kutangaza habari zake, ya kwamba yeye ni mtu wa tatu katika ufalme. Usiku uo huo Belshaza, mfalme wa Wakaldayo, akauawa.”

Ni ukweli usiopingika ya kuwa vidole vile vilikuwa ni vidole vya Mungu wazo hili katika Daniel lilikuwa ni wazo linalofanana kabisa na wazo la kile kidole kilichoandika Sheria za Mungu wakati wa Musa, lakini hapa chanda cha Mungu kinashughulika na mtawala mwenye kiburi na majivuno na dharau kuhusu Maswala ya Mungu, Mungu huwapinga wenye kiburi linapokuja swala la Mtu ana kiburi Roho wa Mungu na utendaji wake unafanya kazi ya kuhukumu na kupinga na wale wanaokataa mambo ya Mungu, wakati mwingine watu wanapingana na watumishi wa Mungu na kufikiri au kudhani kuwa watakuwa salama Mungu hawezi kukubali jambo kama hilo litendeke

Zaburi 105:14-15 “Hakumwacha mtu awaonee, Hata wafalme aliwakemea kwa ajili yao. Akisema, Msiwaguse masihi wangu, Wala msiwadhuru nabii zangu.” Wako watu wanadharau neno la Mungu, wanadharau ibada, wanadharau watumishi wa Mungu, wanadharau wakristo, wanadharau wokovu, wanadharau miujiza, na kila kazi zinazofanywa na Roho Mtakatifu ukweli ni wazi kuwa kidole cha Mungu chanda cha Mungu pia kitahusika katika kuleta hukumu haraka kwa wenye kiburi na majivuno Mungu huwapinga wenye kiburi bali huwapa wanyenyekevu neema.

Kidole cha Mungu na wakati wa Huduma ya Yesu.

Wakati wa Huduma ya Yesu Krito duniani neno chanda cha Mungu linaonekana kutumiwa na Bwana Yesu Kristo mwenyewe, Hii ni baada ya kuwa amemponya kwa muujiza mtu aliyekuwa na pepo bubu na kziwi, Mafarisayo na wapinzani wa Yesu Kristo walikosoa vikali miujiza iliyokuwa ikifanywa na Bwana Yesu na kudai kuwa anatoa pepo na kufanya miujiza kwa nguvu za Belzebuli ona

Mathayo 12:22-24 “Wakati ule akaletewa mtu mwenye pepo, kipofu, naye ni bubu; akamponya, hata yule bubu akanena na kuona. Makutano wote wakashangaa, wakasema, Huyu siye mwana wa Daudi? Lakini Mafarisayo waliposikia, walisema, Huyu hatoi pepo, ila kwa Beelzebuli mkuu wa pepo.”

Katika kuwajibu hoja yao Mafarisayo na wapinzani wa kazi za Mungu Roho Mtakatifu ambaye ndiye nguvu ya utendaji iliyokuwa ikitenda kazi ndani ya Kristo, Yesu alieleza wazi kuwa hakuna ufalme unaweza kujipinga wenyewe na hivyo shetani hawezi kuwatoa mashetani, Bali yeye anayafanya anayoyafanya kwa chanda cha Mungu akimaanisha miujiza yote na kazi zote za utoaji wa pepo ni matokeo ya kazi za Roho Mtakatifu atendaye kazi ndani yake na ndani yetu pia

Luka 11:20 “Lakini, ikiwa mimi natoa pepo kwa kidole cha Mungu, basi ufalme wa Mungu umekwisha kuwajilia.” Mathayo 12:24-28 “Lakini Mafarisayo waliposikia, walisema, Huyu hatoi pepo, ila kwa Beelzebuli mkuu wa pepo. Basi Yesu akijua mawazo yao, akawaambia, Kila ufalme ukifitinika juu ya nafsi yake, hufanyika ukiwa; tena mji au nyumba yo yote ikifitinika juu ya nafsi yake, haitasimama.  Na Shetani akimtoa Shetani, amefitinika juu ya nafsi yake; basi ufalme wake utasimamaje? Na mimi nikitoa pepo kwa Beelzebuli, je! Wana wenu huwatoa kwa nani? Kwa sababu hiyo hao ndio watakaowahukumu. Lakini mimi nikitoa pepo kwa Roho wa Mungu, basi ufalme wa Mungu umekwisha kuwajilia.”

Katika maandiko yote hayo ya injili Yesu anasisitiza kuwa anazifanya kazi za Mungu kwa utendaji wa Mungu ulioko ndani yake chanda cha Mungu, yaani Roho Mtakatifu, hii ndio nguvu ile ile iliyotenda kazi katika muujiza wa kusababisha chawa na ndio nguvu, iliyoandika amri za Mungu katika mbao za mawe, na ndio nguvu iliyoandika hukumu katika ukuta kushughulika na Belshaza, Kidole cha Mungu au chanda cha Mungu ni uweza wa Mungu usio na mipaka ni ngubvu za Mungu ni upako utendao kazi, Hakuna chombo cha kibinadamu kinachoweza kupingana na nguvu za kiungu zitendazo kazi za kiungu, hakuna wachawi wanaweza kushindana na nguvu hizo, hakuna utawala unaweza kupoingana na nguvu hizo, hakuna mwanasayansi anaweza kupinga a na nguvu hizo wala hakuna hekima inayozidi hekima ya Chanda cha Mungu ni chanda cha Mungu ndicho kinachotumika kuponya magonjwa kwa wenye shida za aina mbalimbali na kushughulika na mahitaji yote ya aina binadamu.

Kidole cha Mungu sio tu kinatenda miujiza ya uponyaji, lakini pia kinatangaza rehema na msamaha kwa wenye dhambi na kutukinga na wale waliotukusudia mabaya

Yohana 8:3-8Waandishi na Mafarisayo wakamletea mwanamke aliyefumaniwa katika uzinzi, wakamweka katikati. Wakamwambia, Mwalimu, mwanamke huyu amefumaniwa alipokuwa akizini. Basi katika torati, Musa alituamuru kuwapiga kwa mawe wanawake namna hii; nawe wasemaje? Nao wakasema neno hilo wakimjaribu, ili wapate sababu ya kumshitaki. Lakini Yesu akainama, akaandika kwa kidole chake katika nchi. Nao walipozidi kumhoji, alijiinua, akawaambia, Yeye asiye na dhambi miongoni mwenu na awe wa kwanza wa kumtupia jiwe. Akainama tena, akaandika kwa kidole chake katika nchi.”

Wakati watu wanapoorodhesha list ya dhambi zetu ili tuhukumiwe na Mungu, kidole cha Mungu kinaweza kunadika rehema kwaajili yetu kinaweza kuandika dhambi ya kila mmoja ya wale wanaotushitaki, kidole cha Mungu kina uwezo wa kubatilisha hati za mashitaka wakati wote Neno la Mungu linapoonesha kidole cha Mungu kimehusika mahali lazima tujue kuwa ni uweza wa Mungu ni utendaji wa Mungu Roho Mtakatifu akiwa kazini. Kamwe hatupaswi kuogopa kitu, wala kuhofia kitu. Wala hatupaswi kuwaogopa wale watupingao na kwanza wanaonywa waache kucheza na chanda cha Mungu! Aidha chanda cha Mungu kinahusika na uumbaji kuonyesha utendaji wa Mungu uliokuwako wakati wa uumbaji ona

Zaburi 8:1-3 “Wewe, MUNGU, Bwana wetu Jinsi lilivyo tukufu jina lako duniani mwote! Wewe umeuweka utukufu wako mbinguni; Vinywani mwa watoto wachanga na wanyonyao Umeiweka misingi ya nguvu; Kwa sababu yao wanaoshindana nawe; Uwakomeshe adui na mijilipiza kisasi.Nikiziangalia mbingu zako, kazi ya vidole vyako, Mwezi na nyota ulizoziratibisha;”

Hitimisho

Hivi nilivyo na hivyo ulivyo ni matokeo ya kazi yake Mungu wetu, adui zako wakikutisha waambie hivi nilivyo ni chanda cha Mungu, chanda cha Mungu kinaweza kutuelekeza katika sharia yake, katika hukumu zake, katika utendaji wake wa miujiza, katika utendaji wa nguvu zake na uwezo wake dhidi ya wapinzani wetu, wakati wote tunaweza kumkumbusha Mungu ya kuwa tunahitaji kidole chake kihusike katika kila eneo la maisha yetu na kuleta mpenyo kila amahali pale tunahitaji mpenyo

Na Rev. Innocent Samuel Kamote.

Mkuu wa wajenzi mwenye Hekima.  

Jumamosi, 18 Machi 2023

Msaada na wokovu kwa njia nyingine!


Esta 4:13-14 “Naye Mordekai akawaagiza wampelekee Esta jibu la kusema, Wewe usijidhanie kuwa wewe utaokoka nyumbani mwa mfalme, zaidi ya Wayahudi wote. Kwa maana wewe ukinyamaza kabisa wakati huu, ndipo kutakapowatokea Wayahudi msaada na wokovu kwa njia nyingine; ila wewe utaangamia pamoja na mlango wote wa baba yako; walakini ni nani ajuaye kama wewe hukuujia ufalme kwa ajili ya wakati kama huo?”   


          


Utangulizi.

Katika Historia ya Dunia moja ya watu au jamii au kabila au taifa la watu waliopitia katika mateso na mashambulizi makali sana duniani ni Wayahudi, Wayahudi wamekuwa watu wa kuchukiwa kila mahali Duniani, Mifumo yote ya kishetani duniani, imepangwa na kukusudia kuharibu kabisa mpango wa Mungu kupitia taifa hilo kuanzia na mpango wa ukombozi wa wanadamu ambao ulikuja pia kupitia Yesu Ktisto kupitia taifa hilo, lakini sio hivyo tu hata mpango wa Mungu wa baadaye. 

Katika maisha yetu vilevile wako watu wengine ambao Mungu ana mpango na makusudi makubwa na maisha yao kwaajili ya kuwahudumia watu wengine! Lakini hata hivyo wamekutana na mashambulizi makali sana kutoka kwa watu mbalimbali kwaajili ya kupambana na maisha yao, na kusudi lile ambalo Mungu ameliweka ndani yao, kokote kule waliko wanachukiwa na kupigwa vita nani tamaa ya shetani na maajenti wake kuona watu hao wanaharibikiwa wanakwenda mbali na nyuso zao na hata kuwaua, Mwalimu alisema kwamba sote tutachukiwa kwaajili ya jina lake. 

Yohana 16:1-3 “Maneno hayo nimewaambia, msije mkachukizwa. Watawatenga na masinagogi; naam, saa yaja atakapodhania kila mtu awauaye ya kuwa anamtolea Mungu ibada. Na hayo watawatenda kwa sababu hawakumjua Baba wala mimi.” 

Kama ilivyo kwa wayahudi na wanafunzi wa Yesu Kristo watachukiwa vilevile, na mtu mmoja mmoja kwa kadiri unavyompenda Mungu utachukiwa na wakati mwingine hata na wakristo wenzako, na au hata watumishi wenzako na wakati mwingine hata watu waliokuzidi kila kitu wanaweza kuchukizwa nawe kumbuka maneno ya Paulo mtume “Ndugu za uongo” hawa watakuchukia na kukuonea wivu na kukutengenezea zengwe ili yamkini uharibikiwe na kuangamizwa nah ii ndio furaha yao au kwa ujinga wakidhani wanafanya mapenzi ya Mungu, katika mazingira kama hayo bado tunapaswa kukumbuka kuwa Mungu yupo naye ndiye tumaini letu na tegemeo letu na ya kuwa ataleta msaada na wokovu kwa njia nyingine hata nje ya zile tunazozitegemea! 

Ni ahadi ya Mungu ya kuwa njia moja ikifungwa atafungua na njia nyingine 

1Wakoritho 10:13 “Jaribu halikuwapata ninyi, isipokuwa lililo kawaida ya wanadamu; ila Mungu ni mwaminifu; ambaye hatawaacha mjaribiwe kupita mwezavyo; lakini pamoja na lile jaribu atafanya na mlango wa kutokea, ili mweze kustahimili.” 

Kuujia Ufalme kwa wakati. 

Kitabu cha Esta kiliandikwa kwa makusudi ya kuwafundisha wayahudi sababu ya kuwepo kwa sikukuu ya Purim,  Neno hilo Purim ni neno la Kiibrania ambalo kwa kiingereza ni “LOTS” kwa Kiswahili ni Kura au Muswada, ni sikukuu ya wayahudi kukumbuka au kufurahia ukombozi uliotokea karne tano hivi kabla ya Kristo kwa wayahudi wachache waliokuwa wakikaa huko uajemi ambao walipitishiwa Mswada na ukapigiwa kura kwamba watu wa kabila hilo wauawe, ni kutokana na wokovu mkubwa walioupata ndipo Mordekai akaamuru waikumbuke siku hiyo na kuiadhimisha kokote waliko 

Esta 9:20-26 “Basi Mordekai aliyaandika mambo hayo; naye akapeleka barua kwa Wayahudi wote waliokaa katika majimbo yote ya mfalme Ahasuero, waliokuwa karibu na waliokuwa mbali, kuwaonya wazishike siku ya kumi na nne ya mwezi wa Adari, na siku ya kumi na tano yake, mwaka kwa mwaka, ambazo ni siku Wayahudi walipojipatia raha mbele ya adui zao, na mwezi uliogeuzwa kwao kuwa furaha badala ya huzuni, na kuwa sikukuu badala ya kilio; wazifanye siku hizo ziwe za karamu na furaha, za kupeana zawadi na za kuwapa maskini vipawa. Nao Wayahudi wakakubali kufanya kama walivyoanza, na kama Mordekai alivyowaandikia; kwa sababu Hamani bin Hamedatha, Mwagagi, adui ya Wayahudi wote, alikuwa amefanya shauri juu ya Wayahudi ili kuwaangamiza, akapiga Puri, yaani kura, ili kuwakomesha na kuwaangamiza pia; bali mfalme alipoarifiwa, aliamuru kwa barua ya kwamba hilo shauri baya alilolifanya juu ya Wayahudi limrudie kichwani pake mwenyewe; na ya kwamba yeye na wanawe watundikwe juu ya mti. Hivyo wakaziita siku hizo Purimu, kwa jina la Puri. Basi, kwa ajili ya maneno yote ya barua hiyo, na kwa yale waliyoyaona wenyewe juu ya jambo hilo, na mambo yenyewe yaliyowajia”, 

Katika wakati wa tukio hilo la ukombozi Mungu alikuwa ameinua binti wa kiyahudi akliyeitwa Esta kuwa malikia wa uajemi baada ya kuolewa na aliyekuwa mfalme kwa wakati huo, Mordekai mjomba wake alikuja kumtumia binti huyu kuwa sababu ya wokovu mkubwa wa wayahudi alipokuwa madarakani, kuingia kwake madarakani ulikuwa ni mpango wa Mungu ili kwamba aweze kuja kuwa msaada katika wakati mgumu wa saa ya kujaribiwa kwa Israel nani kupitia yeye kweli Mungu alileta wokovu mkubwa, baada ya Mjomba wake Mordekai kumfunulia mpango mbaya uliokuwa umepitishwa wa kuwaabngamiza wayahudi! Esta alikuwa tayari kuyatoa maisha yake kwaajili ya Ndugu zake kwani ilikuwa ni desturi ngumu kuwa kumuendea mfalme bila kibali chake hata kama wewe ni malikia kungekugharimi kifo isipokuwa kama mfalme atakunyooshea fimbo ya dhahabu 

Esta 4:15-16 “Basi Esta akawatuma ili wamjibu Mordekai,Uende ukawakusanye Wayahudi wote waliopo hapa Shushani, mkafunge kwa ajili yangu; msile wala kunywa muda wa siku tatu, usiku wala mchana, nami na wajakazi wangu tutafunga vile vile; kisha nitaingia kwa mfalme, kinyume cha sheria; nami nikiangamia, na niangamie” 

Kwa nini Esta alikubali kujitoa muhanga kwaajili ya watu wake ni baada ya Mordekai kumjulisha kuwa emekuwepo madarakani katika ufalme ule huenda kwa mpango wa Mungu ili awaletee watu wake wokovu, jambo ambalo pia lilimpa heshima kubwa mwanamke huyu! 

Ni muhimu kufahamu kuwa wako watu ambao wakiingia madarakani wanaweza kugeuka na kuwa Baraka kubwa sana kwa jamii na watu, na wako watu ambao wakiingia madarakani wanaweza kuwa sababu ya majutio makubwa sana kwa wengine, ashukuriwe Mungu kuwa esta alikubali kuwa Baraka kwa wengine, lakini wako viongozi ambao wewe na mimi tutaweza kuendelea kuwakumbuka katika maisha yetu katika mazingira yoyote yale iwe serikalini, au kwenye makanisa yetu, au idara zetu, au kazini kwako au kwenye biashara yako au bosi wako, kwamba wao walipoingia madarakani aidha walikuwa Baraka kubwa sana kwako kiasi ukashukuru na kusema wameujia ufalme kwa wakati, lakini wako viongozi wengine ndio wamekuja wakiwa hawajui kusudi la Mungu ndani yako na wote ni kama wakichukua mazoezi ya kufukuza wanataka kukufukuza wewe, wakitaka kuchukua mazoezi ya umbeya wanakufanyia wewe, wewe ndio unakuwa adui mkubwa wewe ndio unakuwa sababu ya vurugu na vujo na kupitishwa kwa miswada mibaya na mipango mibaya na vita za kila aina hwa ni watu wasiojua kwanini wameujia ufalme na wanadani wameujia ufalme ili wakutoe sadaka wewe wakidhani ya kuwa watajipatia heshima kumbuka Mordekai alimuonya Esta kuwa kama wewe hutatambua wajibu wako wakati huu ndipo utakapowajia wayahudi Msaada na wokovu kwa njia nyingine na wewe na mlango wa baba yako utaangamia, ninawatangazia wote ambao Mungu aliwaweka madarakani ili wawe Baraka kwako na kwangu ya kuwa kama hawajui ni kwa nini wameujia ufalme kwa wakati huu kuwa Mungu atatuletea Msaada na wokovu kwa njia nyingine       nao wataabika katika jina la Yesu! 

Msaada na wokovu kwa njia nyingine! 

Ni muhimu kufahamu kuwa Mungu anatumia watu, na shetani pia anatumia watu, kila mtu aliyeko katika nafasi ya kuwafanyia mema wengine na awafanyie kwa nia njema na nia nzuri,  watu wengi sana wakishapewa nafasi badala ya kuzitumia nafasi hizo kwa kutenda, haki na kuwasaidia watu wa Mungu, kufikia ndoto zao na kutoa msaada wanaingiwa na choyo, wivu, dhuluma, kiburi na kutaka kuabudiwa kama miungu watu, wakati wote wanatafuta Heshima na kama huanguki kuwaabudu wanakasirika sana hiki ndicho kilichowafanya wayahudi kuchukiwa ona 

Esta 3:1-6 “Baada ya hayo mfalme Ahasuero alimwongezea cheo Hamani bin Hamedatha, Mwagagi, akampandisha, akamwekea kiti chake juu ya maakida wote waliokuwapo pamoja naye. Nao watumishi wote wa mfalme, walioketi mlangoni pa mfalme, wakainama na kumsujudia Hamani, maana ndivyo alivyoamuru mfalme kwa habari zake. Bali Mordekai hakuinama, wala kumsujudia. Basi watumishi wa mfalme walioketi mlangoni pa mfalme wakamwambia Mordekai, Mbona wewe waihalifu amri ya mfalme? Ikawa, waliposema naye kila siku asiwasikilize, wakamwarifu Hamani, ili kuona kama mambo yake Mordekai yatasimama; maana alikuwa amewaambia ya kuwa yeye ni Myahudi. Hata Hamani alipoona ya kwamba Mordekai hainami wala kumsujudia, alighadhibika sana. Akaona si shani kumtia mikono Mordekai peke yake; maana wamemjulisha kabila yake Mordekai; kwa hiyo Hamani alitaka kuwaangamiza Wayahudi wote waliokuwa wakikaa katika ufalme wote mzima wa Ahasuero, yaani, watu wake Mordekai.” 

Unaona kwa sababu ya kutaka Heshima na kutaka kuabudiwa Hamani Mwagagi alikasirika sana na kutaka kuona mambo ya Mordekai yatasiamamaje kisa tu kwa mila na desturi za Kiyahudi hawaruhusiwi kutoa heshima ya Mungu kwa wanadamu, wako kina hamani kila kona katika maisha yetu ambao wamevimbaa, wana uchungu, wana hasira wana mipango mibaya imekusudiwa kwaajili yako pale kazini, pale shuleni, pale kwenye biashara, pale jirani, kila mahali wako watu wenye wivu wenye uchungu, wengine wana kila kitu lakini wivu umewajaa, wanatamani kuwa wao tu maisha yao yote, wako watu wengine wana vyeo kibao, kila taasisi yeye ni mtu mkubwa lakini unaweza kushangaa anakufuatilia wewe ambaye huna hata kuku wa mayaini jambo la kushangaza wako watu wanaotaka ukwame, wako wanaotaka uwe masikini, wako wanaotaka usitoke, wako wanaokuroga, wataroga mpaka na watoto wako, wanataka kuhakikisha kuwa kila kitu chako kinaharibika na hufanikiwi na hiyo ndio furaha yao! Hiyo ni roho ya Hamani, ni wao Mungu aliwaweka ili wawe msaada na wokovu katika maisha yako lakini hata kama wao hawako tayari kufanya hay oleo nataka nikutangazie kuwa uko Msaada na wokovu kwa njia nyingine, Mungu atafanya njia pasipo na njia, Mungu atakuinua sana, Mungu atakupeleka juu, sisi ni wale ambao msaada wetu hautoki kwa wanadamu Msaada wetu u katika Bwana aliyezuiumba mbingu na nchi 

Zaburi 121:1-8 “Nitayainua macho yangu niitazame milima, Msaada wangu utatoka wapi? Msaada wangu u katika Bwana, Aliyezifanya mbingu na nchi. Asiuache mguu wako usogezwe; Asisinzie akulindaye; Naam, hatasinzia wala hatalala usingizi, Yeye aliye mlinzi wa Israeli. Bwana ndiye mlinzi wako; Bwana ni uvuli mkono wako wa kuume. Jua halitakupiga mchana, Wala mwezi wakati wa usiku.  Bwana atakulinda na mabaya yote, Atakulinda nafsi yako. Bwana atakulinda utokapo na uingiapo, Tangu sasa na hata milele.” 

Unaona wakati wote na kwa karne nyingi wayahudi na wakristo wametiana moyo kwamba wote wanaopitria magumu wasiwaangalie wanadamu, tunajua kuwa Mungu huwatumia wanadamu lakini na shetani pia huwatumia wanadamu, hivyo tunapopitia hatari na kukawa kuna mtu tyunamtegemea atusaidie mtu huyu anaweza kusahau, Yuko mtu ambaye Yusufu alimtafasiria Ndoto gerezani na akamwambia ya kuwa ndugu yangu utakaporudi katika kiti cha mfalme unikumbuke na mimi maana nimefungwa mahali hapa kwa uonevu lakini mtu huyo alisahau ona 

Mwanzo 40: 13-23 “Baada ya siku tatu Farao atakiinua kichwa chako, atakurudisha katika kazi yako; nawe utampa Farao kikombe mkononi mwake, kama desturi ya kwanza, ulipokuwa mnyweshaji wake. Ila unikumbuke mimi, utakapopata mema, ukanifanyie fadhili, nakuomba, ukanitaje kwa Farao, na kunitoa katika nyumba hii. Kwa sababu hakika naliibiwa kutoka nchi ya Waebrania, wala hapa sikutenda neno lo lote hata wanitie gerezani. Mkuu wa waokaji alipoona ya kwamba hiyo tafsiri ni ya mema, akamwambia Yusufu, Mimi kadhalika nilikuwa katika ndoto yangu, na tazama, ziko nyungo tatu za mikate myeupe juu ya kichwa changu. Na katika ungo wa juu, mlikuwa na kila namna ya chakula kwa Farao, kazi za mwokaji; ndege wakavila katika ungo juu ya kichwa changu. Yusufu akajibu, akasema, Tafsiri yake ndiyo hii Nyungo tatu ni siku tatu. Baada ya siku tatu Farao atakiinua na kukuondolea kichwa chako, na kukutundika juu ya mti, na ndege watakula nyama yako. Ikawa siku ya tatu, siku ya kuzaliwa kwake Farao, akawafanyia karamu watumwa wake wote; akakiinua kichwa cha mkuu wa wanyweshaji, na cha mkuu wa waokaji, miongoni mwa watumwa wake. Akamrudisha mkuu wa wanyweshaji katika kazi yake ya kunywesha, naye akampa Farao kikombe mkononi mwake. Bali akamtundika mkuu wa waokaji, kama Yusufu alivyowafasiria. Lakini huyo mkuu wa wanyweshaji hakumkumbuka Yusufu, alimsahau ” 

Nadhani unaweza kuona mioyo ya kibinadamu, wakati mwingine Mungu anafungua milango na kumuinua mtu ili aweze kuwa baraka kwako lakini badala ya Mtu huyo kuwa Baraka anajibariki yeye, hii ilimtokea Yusufu hata alipotoa maagizo unikumbuke mtu yule alimsahau, Biblia inasema lakini mkuu huyo wa wanyweshaji hakumkumbuka Yusufu , wakati mwingine Mungu atainua Mwanamke au mwanaume  katika mahali Fulani kwa kusudi fulani ili wabebe jukumu Fulani na kuyatimiza mapenzi ya Mungu kwako na wanaweza kujisahau au wanaweza kusaidia lakini yote katika yote ni ili Mungu atimize mpango wako kwake katika maisha yako wakikusahau usisikitike, wakikujali usisikitike Mungu ataleta Msaada na wokovu kwa njia nyingine, Mungu anaweza kumtumia kila mmoja wetu kwa nafasi yake kutimiza mpango wake katika maisha yetu nan i muhimu sana kujiangalia katika kila nafasi tulizo nazo tukijisahau basi tujue wazi ya kuwa makudui ya Mungu hayawezi kuzuilika yeye ataleta Msaada na wokovu kwa njia nyingine na sisi wahusika tunaweza kujikuta tunaaangamia  

Esta 4:14 “Kwa maana wewe ukinyamaza kabisa wakati huu, ndipo kutakapowatokea Wayahudi msaada na wokovu kwa njia nyingine; ila wewe utaangamia pamoja na mlango wote wa baba yako; walakini ni nani ajuaye kama wewe hukuujia ufalme kwa ajili ya wakati kama huo?” 

Baraka Burton katika wimbo wake NAOMBA NIWE BARAKA Anaimba maneno muhimu sana ambayo Mungu ametaka yaaambatane na ujumbe wangu huu! Kama maombi ya sisi kukubali kutumiwa na Mungu kwa nia njema badala ya kuacha Mungu alete Msaada kwa njia nyingine! ~

Wimbo: Naomba niwe Baraka kwa wengine Na Burton King

Na Rev. Innocent Samuel Kamote

Mkuu wa wajenzi Mwenye Hekima!     

Usifanye neno lolote kwa Upendeleo !


1Timotheo 5:21 “Nakuagiza mbele za Mungu, na mbele za Kristo Yesu, na mbele za malaika wateule, uyatende hayo pasipo kuhukumu kwa haraka; usifanye neno lo lote kwa upendeleo.”


 

Utangulizi:

Mojawapo ya agizo Muhimu sana alilopewa Timotheo, Kama mwangalizi wa makanisa yaliyokuwako Efeso katika waraka alioandikiwa na Paulo Mtume Pamoja na maagizo mengine ni pamoja na kuhakikisha kuwa asifanye neno lolote kwa upendeleo, Upendeleo katika nyakati za leo limekuwa mojawapo ya tatizo kubwa sana katika jamii, jambo linalopelekea kutokutendeka kwa haki, kumekuwepo na tatizo la upendeleo kila mahali leo, Katika mazingira ya kibiashara, mazingira ya kisiasa, katika michezo, na hata makanisani, katika familia, ndugu, serikalini na hata kwenye ndoa, Bila ya aibu yoyote leo hii watu wanaweza kufanya upendeleo na kusahau kabisa kuwa kufanya upendeleo ni dhambi nani kinyume na sheria ya kifalme.

Yakobo 2:8-9 “Lakini mkiitimiza ile sheria ya kifalme kama ilivyoandikwa, Mpende jirani yako kama nafsi yako, mwatenda vema. Bali mkiwapendelea watu, mwafanya dhambi na kuhukumiwa na sheria kuwa wakosaji.”            

Sisi kama wakristo tunapaswa kumfuata Kristo kama mfano wetu, Yesu Kristo hakuwahi kupendelea watu, sisi tunaomfuata yeye kamwe hatupaswi kuonyesha upendeleo maandiko yanatukataza kufanya hivyo, kuonyesha upendeleo ni moja ya tatizo kubwa sana katika jamii nani kinyume na haki ya Mungu, kama mtu anasema ni mkristo na anamwamini Mungu na hata kama sio mwamini awaye yote ambaye ana moyo wa kutenda haki hawezi kuruhusu upendeleo.

 Yakobo 2:1 “Ndugu zangu, imani ya Bwana wetu Yesu Kristo, Bwana wa utukufu, msiwe nayo kwa kupendelea watu.”

Kwa bahati mbaya mambo hayako kama maandiko yanavyoagiza, leo hii ili uweze kufanikiwa ni lazima uwe na connection na watu au mtu Fulani, uwe kwenye kundi au chama Fulani, watu wanapendelea watu au kundi Fulani la watu kwa sababu ni ndugu, au ni wa jinsia yake, au ni masikini, au amepokea rushwa au ni wa ukoo wake, au shemeji zake, au ana hadhi Fulani au ana hela, au wanafahamiana kwa muda mrefu na kadhalika hivyo kuna namna watu wanapewa heshima au upendeleo kwa sababu Fulani, Fulani kama uko na upendeleo leo hii ni lazima utubu na kuelewa kuwa upendeleo ni dhambi mbaya kama zilivyo dhambi nyingine! 

Maana ya upendeleo.

Neno upendeleo katika biblia ya kiyunani husomeka kama PROSOPOLEPSIA ambalo kiingereza linasomeka kama FAVORITISM  ambalo maana yake ni “respect of persons” au “to give judgement with the respect of outwards circumstances of a man” pia inaweza kutafasirika kama giving unfair treatment of a person or group on basis of prejudice kwa Kiswahili Upendeleo ni hali ya kutoa haki au kipaumbele kwa mtu asiyestahili kutokana na maslahi ya mtoa haki, ni hali ya kutoa kipaumbele kwa mtu kulingana na mazingira ya nje au ya muonekano, au kuonyesha heshima kwa mtu au kundi la watu katika mtazamo au maoni yasiyo sahihi, au yasiyo sawa kimsingi upendeleo ni sawa na hakimu anayetoa haki mahali pasipostahili haki, au mwamuzi refa anapowapa watu penalty ambayo kimsingi na kiyushahidi haikupaswa kuwa penalty ni tabia ambayo kibiblia haikubaliki na wala haitokani na Mungu wetu  tunaelezwa kuwa Mungu wetu hana upendeleo na watu wa Mungu wanaonywa kutokuwa na Upendeleo kwa sababu zozote zile Yakobo anajaribu kutioa mfano ulio hai kuhusu upendeleo alipokuwa anajaribu kufafanua somo lake kuwa watu wasiwe na upnendeleo ona 

Yakobo 2:2-5 “Maana akiingia katika sinagogi lenu mtu mwenye pete ya dhahabu na mavazi mazuri; kisha akiingia na maskini, mwenye mavazi mabovu; nanyi mkimstahi yule aliyevaa mavazi mazuri, na kumwambia, Keti wewe hapa mahali pazuri; na kumwambia yule maskini, Simama wewe pale, au keti miguuni pangu, je! Hamkufanya hitilafu mioyoni mwenu, mkawa waamuzi wenye mawazo mabovu? Ndugu zangu wapenzi, sikilizeni, Je! Mungu hakuwachagua maskini wa dunia wawe matajiri wa imani na warithi wa ufalme aliowaahidia wampendao? Bali ninyi mmemvunjia heshima maskini. Je! Matajiri hawawaonei ninyi na kuwavuta mbele ya viti vya hukumu?”

Upendeleo sio tabia ya uungu wala haipaswi kuwa tabia ya watu wa Mungu, kama watu wa Mungu wanaonyesha upendeleo je wana tofauti gani na watu wa dunia hii, ni ukweli usiopingika kuwa dunia inatarajia kujifunza kitu kutoka kwa watu wa Mungu na Mungu mwenyewe kama Mungu mwenyewe hana upendeleo wewe unayefanya upendeleo huoni ya kuwa una kesi ya kujibu, Maandiko yanatuelekeza kuwa Mungu hana upendeleo na kuwa tunapaswa kujifunza kutoka kwake na kwa neno lake kisha tuishi sawa na haki ya Mungu!. 

Mungu hana upendeleo!

Matendo ya mitume 10:34-35 “Petro akafumbua kinywa chake, akasema, Hakika natambua ya kuwa Mungu hana upendeleo; bali katika kila taifa mtu amchaye na kutenda haki hukubaliwa na yeye.”

Petro alitambua kuwa Mungu hana upendeleo, kuna wakati ambapo wayahudi walijidhani ya kuwa huenda wao ni wa Muhimu sana kuliko mataifa mengine dhana hii ilijengeka kwao wakasau kuwa Mungu alitaka kuwaandaa wao kama watumishi wake ili kutoka kwao injili ienee kwa mataifa yote , Lakini ni ukweli unaosmama wazi kuwa Mungu hana hati milikia ya mtu Fulani wako watu hudhani ya kuwa Mungu ni wao nan i wa kwao peke yao na hudhani ya kuwa Mungu anawawasikiliza wao tu nisikilize Mungu ni  wa watu wote yeye hana upendeleo wala hapokei uso wa mwanadamu  Mungu husimama upande wa kila mtu atendaye mema bila kujali ni wa kabila gani  ona

Warumi 2:10-11 “bali utukufu na heshima na amani kwa kila mtu atendaye mema, Myahudi kwanza na Myunani pia; kwa maana hakuna upendeleo kwa Mungu.”

Ndugu zangu hakuna kabila, wala mtu wala kiongozi anayeweza kudhani au kufikiri ya kuwa yeye ni wa muhimu sana kuliko wengine, wako watu wengine wamepata nafasi za uongozi na usimamizi wa mambo lakini hawatendi haki ya Mungu, na badala yake wanafanya upendeleo am,bao uko wazi wazi katika jamii au taasisi wanayoiongoza, Mungu anachukizwa wazi na jambo hilo, huo ni uwakilishi mbaya na mbovu wa kumtangaza Kristo, kila mtu aliyemjia Kristio na kubatizwa kwa Mungu ni sawa na hakuna upendeleo.  

Wagalatia 3:27-29 “Maana ninyi nyote mliobatizwa katika Kristo mmemvaa Kristo. Hapana Myahudi wala Myunani. Hapana mtumwa wala huru. Hapana mtu mume wala mtu mke. Maana ninyi nyote mmekuwa mmoja katika Kristo Yesu. Na kama ninyi ni wa Kristo, basi, mmekuwa uzao wa Ibrahimu, na warithi sawasawa na ahadi.”

Unaona maandiko yanaonyesha kuwa sisi wote tumemvaa Kristo, sisi wote tumekuwa wamoja katika Kristo, haijalishi wewe myahudi, au myunani, haijalishi wewe mnyakyusa au mbondei, haijalishi wewe kijana au mzee, haijalishi wewe mtumwa au huru, haijalishi wewe ni wa namna gani sisi sote tunazo ahadi sawasawa na Ibrahimu na Isaka na Yakobo, kama Mungu alimlinda na kumtetea Abrahamu anatafanya hivyo kwa yeyote yule aliyemwamini mwana wake Yesu Kristo laizma ufikie wakati tuache kiburi na majivuno na kudhani kuwa mtu Fulani ana umuhimu sana kwa Mungu kuliko mwingine, Hakuna mtu ambaye anaweza kudhani ya kuwa amefanya makubwa sana kuliko mwingine au labda anasikilizwa sana na Mungu kuliko wengine kama mtu anajiona yuko hivyo nataka nikuambie wazi hicho ni kiburi, Mungu hapokei uso wa mwanadamu wala hapokei rushwa ona

Kumbukumbu la Torati 10:17 “Kwa maana Bwana, Mungu wenu, yeye ndiye Mungu wa miungu, na Bwana wa mabwana, Mungu mkuu, mwenye kuogofya, asiyependelea nyuso za watu, wala hakubali rushwa”.

Wakati mwingine tumeona watu wakitetewa waziwazi tena waliostahili hukumu tena wakiwa hawajatubu lakini kwa sababu wanajuana na wakubwa wanapewa upendeleo, kwa sababu wana connection wako tu, kuna watu ambao walifanya makosa madogo tu na wamehukumiwa vikali, kuna watu wana makosa makubwa lakini wako, kuna watu wako magerezani kwa sababu ya kusingiziwa tu, kuna watu kwa sababu wanachukiwa wanatafutiwa makosa hata ya kupakaziwa tu ili wahukumiwe hii ni tabia mbaya ya kibinadamu nadhani hakuna mtu ambaye ameishi kwenye jamii yenye upendeleo ambaye anaweza kuwa na furaha, wana michezo ambao timu zao wakati mwingine zimechezeshwa na marefarii wabaya wameonekana kukata tama sana pale timu nyingine inapobebwa na juhudi za wale waliotumia nguvu zao na akili zao zikipuuzwa na kutokuonekana kuwa kitu hapo ndipo utakapoelewa kuwa upendeleo sio kitu kizuri, katika ndoa vilevile pale ambapo wazazi wa upande mmoja wameonekana kupewa kipaumbele kuliko wazazi wa upande mwingine zimekuwa ni chachu na changamoto zenye kukatisha tamaa sana katika familia mbalimbali narudia tena hakuna mtu anayeweza kuwa na furaha na amani pale udhalimu wa upendeleo unapofanyika katika jamii yake, unakwenda mahakamani mahali ambapo unatarajia utapokea haki na unakuta hukumu inapotoshwa je unaweza kuwa na furaha na sehemu hiyo? Mwalimu anaposahihisha na kumuongezea marks mwanafunzi ambaye hakustahili je unaweza kufurahia kuweko katika jamii yenye upendeleo? Ashukuriwe Mungu hana upendeleo kwa Mungu kila mtu atahukumiwa sawa na matendo yake bila upendeleo ona

Wakolosai 3:23-25 “Lo lote mfanyalo, lifanyeni kwa moyo, kama kwa Bwana, wala si kwa wanadamu, mkijua ya kuwa mtapokea kwa Bwana ujira wa urithi. Mnamtumikia Bwana Kristo. Maana adhulumuye atapata mapato ya udhalimu wake, wala hakuna upendeleo.”

Unapofanya upendeleo unaweza kudhani kama sio dhambi hivi, lakini ni ukweli ulio wazi kuwa unapofanya upendeleo unafanya dhuluma, unadhulumu wanaostahili, kwa wasiostahili, maandiko yanaonya kuwa adhulumuye atapata mapato ya udhalimu wake wala hakuna upendeleo,  ni Muhimu kwa kila mtu aliye katika nafasi ya maamuzi akajifunza kutenda kwa haki na kumcha Mungu Mungu anataka watu wote watendewe haki na kamwe kusiwe na aina yoyote ya upendeleo unaoshakiziwa na jambo lolote lile kifedha au uso wa mwanadamu ona

 2Nyakati 19:5 -7 “Akasimamisha makadhi katika nchi, katikati ya miji yote yenye maboma ya Yuda, mji kwa mji; akawaambia hao makadhi, Angalieni myafanyayo; kwa kuwa hammfanyii mwanadamu hukumu, ila Bwana; naye yupo pamoja nanyi katika neno la hukumu. Basi sasa hofu ya Bwana na iwe juu yenu; angalieni mkaifanye; kwa maana kwa Bwana, Mungu wetu, hapana uovu, wala kujali nafsi za watu, wala kupokea zawadi.”

Usifanye neno lolote kwa Upendeleo !

Nyakati za Kanisa la kwanza walijitahidi sana kuhakikisha kuwa wanakuwa mbali na upendeleomoja ya changamoto kubwa za kibinadamu zilizojitiokeza mapema nyakati za kanisa la kwanza ni pamoja na upendeleo jambo lililopeleka Mitume kuwa makini katika uchaguzi wa viongozi na mashemasi ambao kimsingi walipaswa kuwa watu wa haki watu wasio na upendeleo ona

Matendo 6:1-7 “Hata siku zile wanafunzi walipokuwa wakiongezeka hesabu yao, palikuwa na manung'uniko ya Wayahudi wa Kiyunani juu ya Waebrania kwa sababu wajane wao walisahauliwa katika huduma ya kila siku. Wale Thenashara wakawaita jamii ya wanafunzi, wakasema, Haipendezi sisi kuliacha neno la Mungu na kuhudumu mezani. Basi ndugu, chagueni watu saba miongoni mwenu, walioshuhudiwa kuwa wema, wenye kujawa na Roho, na hekima, ili tuwaweke juu ya jambo hili; na sisi tutadumu katika kuomba na kulihudumia lile Neno. Neno hili likapendeza machoni pa mkutano wote; wakamchagua Stefano, mtu aliyejaa imani na Roho Mtakatifu, na Filipo, na Prokoro, na Nikanori, na Timoni, na Parmena, na Nikolao mwongofu wa Antiokia; ambao wakawaweka mbele ya mitume, na walipokwisha kuomba wakaweka mikono yao juu yao. Neno la Mungu likaenea; na hesabu ya wanafunzi ikazidi sana katika Yerusalemu; jamii kubwa ya makuhani wakaitii ile Imani.”              

Haki inapotendeka katika jamii kunakuwa na baraka kubwa sana, lakini dhuluma inapotendeka watu huwa na manung’uniko Mungu anawataka watu wake wote kuwa mstari wa mbele katika kutenda haki na ndio maana utaweza kuona katika mstari wa Msingi Paulo akiagiza kwa kiapo akimwapisha Timotheo mbele za Mungu na mbele za malaika asifanye neno lolote kwa upendeleo hili sio agizo la mchezo maana yake Mungu na malaika mbinguni wanatutazamia tutende haki na huku ya Mungu iko pale pale kwa wasiotenda haki

1Timotheo 5:21 “Nakuagiza mbele za Mungu, na mbele za Kristo Yesu, na mbele za malaika wateule, uyatende hayo pasipo kuhukumu kwa haraka; usifanye neno lo lote kwa upendeleo.”

Rev. Innocent Samuel Kamote

Mkuu wa wajenzi Mwenye Hekima!