Waefeso 4:11-12 “Naye alitoa wengine kuwa
mitume, na wengine kuwa manabii; na wengine kuwa wainjilisti na wengine kuwa
wachungaji na waalimu; kwa kusudi la kuwakamilisha watakatifu, hata kazi ya
huduma itendeke, hata mwili wa Kristo ujengwe;”
Utangulizi
Shule ya huduma ni mafundisho
maalumu ya kibiblia yaliyoandaliwa na Rev. Innocent Samuel Kamote kwa kusudi la
kuwaadaa watu wa Mungu kuwa tayari kwaajili ya huduma za kichungaji ndani ya
kanisa, huduma za kikanisa, na huduma zote za kiroho kupita mafundisho ya
Biblia, mafundisho haya huandaliwa kwa programu maalumu zinazolingana na maono
ya kanisa letu na mtindo ambao sisi tumechagua kumtumikia Mungu kwa huo, Ni
muhimu kujikumbusha kuwa kusudi kubwa la Mungu kutuokoa sio kwaajili ya
kuhudhuria ibada makanisani pekee bali kwaajili ya kumtumikia yeye, Mungu
anachukizwa sana na wakristo waliodumaa kiroho ambao anawatarajia labda
wangelikuwa walimu wa wengine lakini kwa kutokufahamu wao wamebaki kuwa
wachanga kwa miaka mingi sasa.
Waebrania 5:11-14 “Ambaye tuna maneno mengi
ya kunena katika habari zake; na ni shida kuyaeleza kwa kuwa mmekuwa wavivu wa
kusikia. Kwa maana, iwapasapo kuwa waalimu, (maana wakati mwingi umepita),
mnahitaji kufundishwa na mtu mafundisho ya kwanza ya maneno ya Mungu; nanyi
mmekuwa mnahitaji maziwa wala si chakula kigumu. Kwa maana kila mtu atumiaye
maziwa hajui sana neno la haki, kwa kuwa ni mtoto mchanga. Lakini chakula
kigumu ni cha watu wazima, ambao akili zao, kwa kutumiwa, zimezoezwa kupambanua
mema na mabaya.”
Mungu anapotuokoa anataka
tuimarike kwanza kiroho na kisha baada ya kuimarika atutumie sisi kuimarisha
wengine, kwa hiyo Mungu hutukuza na kutukomaza kiroho, ili tuje tumtumikie na
kuhakikisha kuwa kazi ya huduma inatendeka, kwa hiyo kila mtu aliyeokoka
anapaswa kukua na kufikia ngazi ya kuwa mtenda kazi yaani watu wanaowahudumia
wengine katika mwili wa Kristo, sio mpango wa Mungu wewe ubaki kama ulivyo kila
mwaka!
Luka 22:31-32 “Akasema, Simoni, Simoni,
tazama, Shetani amewataka ninyi apate kuwapepeta kama vile ngano; lakini
nimekuombea wewe ili imani yako isitindike; nawe utakapoongoka waimarishe ndugu
zako.”
Leo tunapochukua muda kuzama kwa
kina na mapana na marefu katika kujifunza shule hii maalumu ya huduma, Mungu
anataka kukuimarisha na kuleta ufahamu na ukomavu kwako ili wewe uweze kuwa
msimamizi wa roho za watu ndani ya kanisa letu na kuwasaidia wengine,
tutajifunza somo hili shule ya huduma
kwa kuzingatia vipengele vikuu muhimu vitatu vifuatayo:-
- Sifa za mwanafunzi wa shule ya huduma.
- Umuhimu wa kuwa na uzoefu katika
huduma.
- Mambo yatupasayo kufanya kama wahudumu
katika kanisa.
Sifa za mwanafunzi wa shule ya huduma.
Nyakati za kanisa la kwanza
walipochagua watenda kazi walikuwa makini sana kuzingatia sifa za wale
waliowachagua walijua kuwa wale watakaochaguliwa au kuteuliwa kusaidia
kazi mbalimbali wana sifa na vigezo vyenye kuwafaa sana na kuwa wanaaminika na
ni wanyenyekevu na watii ambao kupitia wao wataisaidia kazi ya Mungu, na
kuwasaidia watu wote walioamini kusimama imara katika Bwana na kuwafundisha
wengine kuishika imani vile vile kama wao walivyofundishwa, tunaona kwa mfano
Paulo Mtume alimchagua Timotheo mtu ambaye alikuwa anaheshimika sana katika Kanisa kutokana na usafi wa Imani yake na sifa zake
zilijulikana na watu wote wa makanisa yaliyokuwako Listra na Ikonio na baada ya
kuongezeka kwake makanisa yakatiwa nguvu katika imani ona:-
Matendo 16:1-5 “Basi akafika Derbe na
Listra, na hapo palikuwa na mwanafunzi mmoja jina lake Timotheo, mwana wa
mwanamke Myahudi aliyeamini; lakini babaye alikuwa Myunani. Mtu huyo
alishuhudiwa vema na ndugu waliokaa Listra na Ikonio.Paulo akamtaka huyo
afuatane naye, akamtwaa akamtahiri kwa ajili ya Wayahudi waliokuwako pande
zile; kwa maana wote walijua ya kuwa babaye ni Myunani. Basi walipokuwa
wakipita kati ya miji ile, wakawapa zile amri zilizoamriwa na mitume na wazee
walioko Yerusalemu, ili wazishike. Makanisa yakatiwa nguvu katika ile Imani,
hesabu yao ikaongezeka kila siku.”
Ni imani yangu kuwa kila
aliyechaguliwa/atakayechaguliwa kuingia katika shule hii ya huduma atakuwa mtii,
atakuwa mnyenyekevu, atafuatilia kwa makini mafundisho yetu, na kujitahidi sana
kuwa na sifa zinazohitajika sawa na maandiko ili aweze kutumika kwa uaminifu na
kupitia wewe makanisa yetu yakatiwe nguvu na kuimarika lakini sio hivyo tu
hesabu ya watu wa makanisa yetu
ikaongezeke kila iitwapo leo. Sasa basi mwanafunzi wa shule ya huduma anapaswa
kuwa na sifa hizi kama neno la Mungu lisemavyo:-
- Kulishika neno la Mungu kama
ulivyofundishwa – Mwanafunzi wa shule ya huduma anapaswa kuwa mtu
anayeyaamini mafundisho yetu kuyakubali, kuyashahika na kuyafuata vile vile
kama alivyofundishwa, mtu hawezi kuwa mwanafunzi wa mtu ambaye hayashiki
mafundsho yake, mwanafunzi wetu ni lazima atusome, asome nia ya mitume wa
kanisa kuwa wanataka nini wana maono gani na wanaelekea wapi, wanaamini
nini, Misingi ya imani yetu ni ipi, kisha aanze kuishi sawa na kile
alichojifunza kutoka kwetu na kukisimamia/tetea
Yohana 8:31-32 “Basi Yesu akawaambia wale Wayahudi waliomwamini, Ninyi
mkikaa katika neno langu, mmekuwa wanafunzi wangu kweli kweli; tena mtaifahamu
kweli, nayo hiyo kweli itawaweka huru.”
Yohana 14:23-24 “Yesu akajibu, akamwambia, Mtu akinipenda, atalishika neno
langu; na Baba yangu atampenda; nasi tutakuja kwake, na kufanya makao kwake.
Mtu asiyenipenda, yeye hayashiki maneno yangu; nalo neno mnalolisikia silo
langu, ila ni lake Baba aliyenipeleka.”
Tito 1:7-9 “Maana imempasa askofu awe mtu asiyeshitakiwa neno, kwa
kuwa ni wakili wa MUNGU; asiwe mtu wa kujipendeza nafsi yake, asiwe mwepesi wa
hasira, asiwe mlevi wala mgomvi, asiwe mpenda mapato ya aibu. Bali awe mkaribishaji,
mpenda wema, mwenye kiasi, mwenye haki, mtakatifu, mwenye kudhibiti nafsi yake;
akilishika lile neno la imani vile vile kama alivyofundishwa, apate kuweza
kuwaonya watu kwa mafundisho yenye uzima, na kuwashinda wenye kupinga.”
2Yohana 1:9-10 “Kila apitaye cheo, wala asidumu katika mafundisho ya
Kristo, yeye hana Mungu. Yeye adumuye katika mafundisho hayo, huyo ana Baba na
Mwana pia. Mtu akija kwenu, naye haleti mafundisho hayo, msimkaribishe nyumbani
mwenu, wala msimpe salamu.”
Mwanafunzi wetu ni lazima awe yule anayeyashika mafundisho
ya Kristo, awe mtu aliyeiva katika neno la Mungu, amejaa neno, analijua neno
analipenda anamoyo wa kujifunza na mwenye sifa za kumpenda Yesu huyu anaweza
kwenda na kile ambacho Kristo amekikusudia akilishika neno la imani vilevile
kama alivyofundishwa!.
- Awe mwaminifu – Kila mwanafunzi
ambaye amechaguliwa au kuteuliwa katika shule ya huduma anapaswa kujifunza
kuwa mwaminifu, Imani yangu ni kuwa kila ambaye yuko katika darasa hili
atakuwa mwaminifu, na kama hauna uaminifu utaomba Mungu sasa akupe kuwa
mwaminifu, Mungu anakuleta katika darasa hili ili akukabidhi injili, na
injili inapaswa kukabidhiwa kwa watu waaminifu ambao wana sifa ya
kuikabidhi kwa wengine, uaminifu huu unaanzia katika kuhudhuria ibada,
zote kufika katika mafundisho ya neno la Mungu, kuandika na kukua kiroho,
na kuwa tayari kuyapeleka hayo
katika makanisa yetu yote na nje ya makanisa yetu ili kujenga umoja na
afya ya kiroho inayofanana vile
vile sawa na ile aliyotuachia Kristo
na mitume wa Bwana
Matendo 2:41-42 “Nao waliolipokea neno lake wakabatizwa; na siku ile
wakaongezeka watu wapata elfu tatu. Wakawa wakidumu katika fundisho la mitume,
na katika ushirika, na katika kuumega mkate, na katika kusali.”
2Timotheo 2:2 “Na mambo yale uliyoyasikia kwangu mbele ya mashahidi
wengi, hayo uwakabidhi watu waaminifu watakaofaa kuwafundisha na wengine.”
1Wakorintho 4:1-2 “Mtu na atuhesabu hivi, kuwa tu watumishi wa Kristo, na
mawakili wa siri za Mungu. Hapo tena inayohitajiwa katika mawakili, ndiyo mtu
aonekane kuwa mwaminifu.”
Mathayo 24:45-47 “Ni nani basi yule mtumwa mwaminifu mwenye akili, ambaye
bwana wake alimweka juu ya nyumba yake, awape watu chakula kwa wakati wake?
Heri mtumwa yule, ambaye bwana wake ajapo atamkuta akifanya hivyo. Amin, nawaambieni, atamweka juu ya vitu vyake
vyote.”
- Awe na unyenyekevu – Tunapoingia
katika shule ya huduma kama hivi, tunaandaliwa kwa lengo, nia na makusudi
ya kuwatumikia watu, watu ndio mtaji wetu mkubwa na sio vinginevyo,
tunataka roho zao tuzipeleke kwa Kristo kwa ibada na utumishi wake, kwa hiyo ni lazima tujifunze unyenyekevu,
hatuendi kuwa mabwana wakubwa tunakwenda kuwahudumia watu, Unyeyekevu
unapaswa kuwa kama vazi letu iwe ni tabia yetu inayotutambulisha kila
mahali, mavazi humtambulisha mtu, watumishi wa Kristo wanapaswa
kutambulika kwa unyenyekevu wao kwa sababu ndivyo Bwana wetu Yesu
alivyokua na sisi tu mawakili wake
Wakolosai 3:12-14 “Basi, kwa kuwa mmekuwa wateule wa Mungu, watakatifu
wapendwao, jivikeni moyo wa rehema, utu wema, unyenyekevu, upole, uvumilivu,
mkichukuliana, na kusameheana, mtu akiwa na sababu ya kumlaumu mwenzake; kama
Bwana alivyowasamehe ninyi, vivyo na ninyi. Zaidi ya hayo yote jivikeni upendo,
ndio kifungo cha ukamilifu.”
Wafilipi 2:5-8 “Iweni na nia iyo hiyo ndani yenu ambayo ilikuwamo pia
ndani ya Kristo Yesu; ambaye yeye mwanzo alikuwa yuna namna ya Mungu, naye
hakuona kule kuwa sawa na Mungu kuwa ni kitu cha kushikamana nacho; bali
alijifanya kuwa hana utukufu, akatwaa namna ya mtumwa, akawa ana mfano wa
wanadamu; tena, alipoonekana ana umbo kama mwanadamu, alijinyenyekeza akawa mtii
hata mauti, naam, mauti ya msalaba.”
1Petro 5:2-5 “lichungeni kundi la Mungu lililo kwenu, na kulisimamia,
si kwa kulazimishwa, bali kwa hiari kama Mungu atakavyo; si kwa kutaka fedha ya
aibu, bali kwa moyo. Wala si kama wajifanyao mabwana juu ya mitaa yao, bali kwa
kujifanya vielelezo kwa lile kundi. Na Mchungaji mkuu atakapodhihirishwa,
mtaipokea taji ya utukufu, ile isiyokauka. Vivyo hivyo ninyi vijana, watiini
wazee. Naam, ninyi nyote jifungeni unyenyekevu, mpate kuhudumiana; kwa sababu
Mungu huwapinga wenye kiburi, lakini huwapa wanyenyekevu neema.”
- Awe kielelezo – Katika shule ya
huduma kila mwanafunzi anapaswa kudhamiria kuwa kielelezo chema katika
Imani yetu na mafundisho yetu, Mungu anapoona kuwa sote tumedhamiria kuwa
kielelezo kwa wale watakaoamini ataendelea kutuamini na kutuletea watu
wengi zaidi, kwa sababu wanafunzi huigiza kila kitu kinachofanywa na
walimu wao, wale tunaowahudumia wataigiza kila kitu kutoka kwetu hivyo
neno la Mungu linasiistiza tuwe kielelezo yaani mfano wa kuigwa, wakristo
wote watuigize sisi watuone ndio wa kuigizwa na sio wakrito pekee bali
kila mahali katika jamii tuwe mfano bora wa kuigwa kwa tabia na mwenendo.
Neno kuwa kielelezo katika maandiko ya Kiyunani linatajwa kama neno “tupos” ambalo kwa kiingereza ni “a model for imitation” sawa na mfano wa kuigwa au kielelezo katika
Imani, kila muhudumu anapaswa kuwa kielelezo katika usemi, mwenendo imani na
usafi hakuna namna ya kukwepa jambo hili.
Tito 2:7-8 “katika mambo yote ukijionyesha wewe mwenyewe kuwa
kielelezo cha matendo mema, na katika mafundisho yako ukionyesha usahihi na
ustahivu, na maneno yenye uzima yasiyoweza kuhukumiwa makosa, ili yule mwenye
kupinga atahayarike, kwa kuwa hana neno baya la kunena juu yetu.”
1Timotheo 4:12 “Mtu awaye yote asiudharau ujana wako, bali uwe kielelezo
kwao waaminio, katika usemi na mwenendo, na katika upendo na imani na usafi.”
1Wathesalonike 1:4-7
“Kwa maana, ndugu mnaopendwa na Mungu, twajua
uteule wenu; ya kwamba injili yetu haikuwafikia katika maneno tu, bali na
katika nguvu, na katika Roho Mtakatifu, na uthibitifu mwingi; kama vile
mnavyojua jinsi zilivyokuwa tabia zetu kwenu, kwa ajili yenu. Nanyi mkawa
wafuasi wetu na wa Bwana, mkiisha kulipokea neno katika dhiki nyingi, pamoja na
furaha ya Roho Mtakatifu. Hata mkawa kielelezo kwa watu wote waaminio katika
Makedonia, na katika Akaya.”
- Nidhamu – Ni muhimu kufahamu kuwa
kamwe huwezi kumtenganisha mwanafunzi na maswala ya nidhamu, wanafunzi wa
Yesu ni lazima wawe na nidhamu, hii ni sawa na kujitia nidhamu, kuwa na
kiasi, kujidhibiti, Neno nidhamu katika kiingereza linatamkwa “Discipline” ambalo kwaa asili
linatokana na neno la Kilatini
“Discipulus” ambalo maana yake ni “leaner”
au “Student” hii ndio maana ya mzizi wa neno “Disciples” yaani wanafunzi, kwa msingi huo wanafunzi ni watu
wanaojitawala, wanaojitia nidhamu, kama tunataka kumtumikia Mungu kwa
kiwango kikubwa na kumpa Mungu nafasi ya kututumia lazima tujitie nidhamu,
maisha matakatifu yanahitaji
nidhamu, maombi yanahitaji nidhamu, kujisomea neno kunahitaji nidhamu,
kutunza upako kunahitaji nidhamu, kufunga kunahitaji nidhamu, kuabudu
kunahitaji nidhamu.
1Wakorintho 9:24-27.
“Je! Hamjui, ya kuwa wale washindanao kwa kupiga
mbio, hupiga mbio wote, lakini apokeaye tuzo ni mmoja? Pigeni mbio namna hiyo,
ili mpate. Na kila ashindanaye katika michezo hujizuia katika yote; basi hao
hufanya hivyo kusudi wapokee taji iharibikayo; bali sisi tupokee taji
isiyoharibika. Hata mimi napiga mbio vivyo hivyo, si kama asitaye; napigana
ngumi vivyo hivyo, si kama apigaye hewa; bali nautesa mwili wangu na
kuutumikisha; isiwe, nikiisha kuwahubiri wengine, mwenyewe niwe mtu wa
kukataliwa.”
- Upendo kwa watu – Kuna uhusino
mkubwa sana kati ya kuhudumia watu na upendo, huduma zote zinazohusisha
kuwahudumia watu zinahitaji uwe na upendo, na wala usiwe na ubinafsi, na unapaswa
kuwa na huruma kwa watu, upendo huu sio wa hisia wala wa kinafiki ni utendaji wa kivitendo
unaohusisha kukutana na mahitaji ya wengine, kwa hiyo muda wetu, vipawa
vyetu tunawekeza katika kuhakikisha tunawahudumia watu kwa huruma na
upendo
Mathayo 9:35-38 “Naye Yesu alikuwa akizunguka katika miji yote na vijiji,
akifundisha katika masinagogi yao, na kuihubiri habari njema ya ufalme, na
kuponya magonjwa yote na udhaifu wa kila aina. Na alipowaona makutano,
aliwahurumia, kwa sababu walikuwa wamechoka na kutawanyika kama kondoo wasio na
mchungaji. Ndipo alipowaambia wanafunzi wake, Mavuno ni mengi, lakini watenda
kazi ni wachache. Basi mwombeni Bwana wa mavuno, apeleke watenda kazi katika
mavuno yake.”
Umuhimu wa kuwa na uzoefu katika huduma
Ni muhimu kufahamu kuwa nyakati
za kanisa la kwanza walipotaka kuchagua mtu katika huduma mojawapo ya msingi
waliouzingatia ulikuwa ni uzoefu katika huduma, jambo hili lilikubalika na
jamii yote ya wanafunzi, kumtumikia Mungu na kutumikia watu linahesabiwa kama
jambo la furaha katika Kristo na sio mzigo kwa sababu iliaminika kama njia ya
kujiweka karibu na Mungu huku ukitimiza kazi hii njema ya kiungu
Matendo 1:21-26 “Basi katika watu
waliofuatana nasi wakati wote Bwana Yesu alipokuwa akiingia na kutoka kwetu,
kuanza tangu ubatizo wa Yohana, hata siku ile alipochukuliwa kwetu kwenda juu,
inapasa mmoja wao awe shahidi wa kufufuka kwake pamoja nasi. Wakaweka wawili,
Yusufu, aitwaye Barsaba, aliyekuwa na jina la pili Yusto, na Mathiya. Kisha
wakaomba, wakasema, Wewe, Bwana, ujuaye mioyo ya watu wote, tuonyeshe ni nani
uliyemchagua katika hawa wawili, ashike mahali katika huduma hii na utume huu,
alioukosa Yuda, aende zake mahali pake mwenyewe. Wakawapigia kura; kura
ikamwangukia Mathiya; naye akahesabiwa kuwa pamoja na mitume kumi na mmoja.”
Tunapozungumzia uzoefu hapa
tunamaanisha mtu aliyekaa katika mafundisho ya Bwana Yesu kwa muda wa kutosha
au aliyepitia shule zote muhimu zinazohusiana na utumishi huu tulioitiwa, kwa
maana nyingine hapaswi kuwa mtu aliyeokoka hivi karibuni au aliyepandishwa kwa
haraka haraka, kanisa la sasa lina watu wengi walioibuka kama uyoga, mtu
alikuwa mganga wa kienyeji, mchawi, sheikh hata hajakaa sawa tayari kesho
unasikia ni mhudumu
1Timotheo 3:6-7 “Wala asiwe mtu aliyeongoka
karibu, asije akajivuna akaanguka katika hukumu ya Ibilisi. Tena imempasa
kushuhudiwa mema na watu walio nje; ili asianguke katika lawama na mtego wa
Ibilisi.”
Kanisa linalotaka uamsho mzito na wa kudumu halina budi kwenda na msingi huu,
ambapo neno la Mungu linaonya kuwa hatupaswi kumchagua mtu katika huduma ambaye
bado ni mchanga, kumpaisha mtu kwa haraka kunaweza kutuletea madhara makubwa
kutokana na kuwa mtu huyo anaweza asiwe na uzoefu wa ukomavu wa kiroho, kwa
hiyo kumuinua mtu kwa haraka kunaweza kumletea kiburi na majivuno na anguko la
haraka pia kama Shetani alivyoanguka kwa majivuno, kwa hiyo mwanafunzi
anayeandaliwa kuwa mhudumu wa injili anapawa kuwa mtu mzima kiroho mtu
aliyepitishwa na Mungu katika shule mbalimbali na sio kwa sababu ya kipawa
chake kuepusha hatari ya kuwa na
majivuno kwa hiyo asiwe mtu mchanga au aliyeinuka haraka “Novice” kwa Kiyunani “neophutos” maana yake kwa kingereza
ni “Newly planted” yaani pandikizi
jipya mtu ambaye hana ukomavu katika imani, kwa hiyo anaweza kuwa ameokoka hivi
karibuni, au akawa mtu ambaye amedumaa kiroho, ndio maana siku hizi unaweza
kuona mtu ni Askofu lakini ana bifu na mtu fulani, anabagua ana mtu ana uadui
naye, ana uchungu, na ugomvi na kupoozesha kabisa sifa zinazomuonyesha kuwa ni
mwanafunzi wa Yesu, makanisa mengi yamepoteza mwelekeo pale yalipowababaikia
watu kwa sababu walikuwa Masheihk, au Wasomi, au wenye vyeo vikubwa na bila
kupitia michakato kadhaa ya kiimani wakapaishwa kuwa viongozi wa kanisa na hii
imechangia kuilifanya kanisa kupoa na kuwa na watu wenye kutumia akili zao
zaidi kuliko hata kumsikiliza Mungu Roho Mtakatifu japo tunahitaji uwiano.
Onyo la kutokuweka viongozi
wachanga katika kanisa linatolewa katika misingi mikuu minne ya tahadhari:-
- Kuanguka katika mtego wa ibilisi kuwa
na kiburi
- Kuitia aibu kanisa kutokana na kukosa
ukomavu na mizizi ya kiimani
- Kukosekana kwa msimamo katika mafundisho
na kushindwa kuisimamia imani au kuitetea
- Kwamba bado anahitaji ukomavu katika
wokovu,mafundisho na tabia, ukomavu wa hekima na busara
Matendo 6:3-4 “Basi ndugu, chagueni watu
saba miongoni mwenu, walioshuhudiwa kuwa wema, wenye kujawa na Roho, na hekima,
ili tuwaweke juu ya jambo hili; na sisi tutadumu katika kuomba na kulihudumia
lile Neno.”
Ukomavu wa kiroho ni mchakato
unachukua muda, wokovu ni mara moja lakini kujengeka kiroho ni safari
inayohitaji mchakato wa muda mpaka mtu akue afikie hatua ya kuweza kula chakula
kigumu, wakati mtoto mchanga kiroho anahitaji maziwa na huduma ya kichungaji,
mtoto mdogo anahitaji malezi na sio kubebeshwa mzigo, kuwabebesha watoto
wachanga kiroho mzigo wa uongozi ni kutafuta kuwadhuru na kuwaharibu na pia
kuliharibu kanisa, unaweza kuwafanya wawe na kiburi na majivuno, unaweza
kusababisha imani yao ikaharibika, unaweza kuwafanya wakakata tamaa,angalau mtu
awe amedumu katika Imani na mafundisho kwa muda usiopungua miaka mitatu kama
alikuwa mwaminifu kuhuduhria ibada na mafundisho ya kanisa letu, anaijua imani
yetu na anauwezo wa kuitetea.
Waebrania 5:14 “Lakini chakula kigumu ni
cha watu wazima, ambao akili zao, kwa kutumiwa, zimezoezwa kupambanua mema na
mabaya.”
1Wakorintho 3:1-2 “Lakini, ndugu zangu,
mimi sikuweza kusema nanyi kama na watu wenye tabia ya rohoni, bali kama na
watu wenye tabia ya mwilini, kama na watoto wachanga katika Kristo.
Naliwanywesha maziwa sikuwalisha chakula; kwa kuwa mlikuwa hamjakiweza. Naam,
hata sasa hamkiwezi,”
1Timotheo 3:8-10 “Vivyo hivyo mashemasi na
wawe wastahivu; si wenye kauli mbili, si watu wa kutumia mvinyo sana, si watu
wanaotamani fedha ya aibu. Wakiishika siri ya imani katika dhamiri safi.Hawa
pia na wajaribiwe kwanza; baadaye waitende kazi ya shemasi, wakiisha kuonekana
kuwa hawana hatia.”
Mambo yatupasayo kufanya kama wahudumu katika kanisa.
Kila mwanafunzi wa shule ya
huduma anapaswa kufahamu kuwa ameitwa kuutumikia mwili wa Kristo huu ni utu
mishi mwema sana na wa hali ya juu na kama kila mmoja atakuwa mwaminifu Mungu
atampa thawabu, kwa hiyo huduma hii iko kwaajili ya kufaidiana yaani kuujenga
mwili wa Kristo na sio kushindana na uongozi, bali kusaidia.
1Wakorintho 12:4-7 “Basi pana tofauti za
karama; bali Roho ni yeye yule. Tena pana tofauti za huduma, na Bwana ni yeye
yule. Kisha pana tofauti za kutenda kazi, bali Mungu ni yeye yule azitendaye
kazi zote katika wote. Lakini kila mmoja hupewa ufunuo wa Roho kwa kufaidiana.”
Neno kufaidiana katika maandiko
ya kiyunani linatumika neno “Sumpherō” ambalo kwa kiingereza linatumika
neno “Contribute” sawa na kuchangia kwa faida kama vile Paulo
alivyosema mahali Fulani mmoja alipanda mwingine akatia maji bali mwenye kukuza
ni Mungu, Mungu ametupa huduma na akili na vipawa mbalimbali ili viweze
kuchangia katika kuujenga mwili wa Kristo ambao kimsingi hauwezi kujengwa na
mtu mmoja kwa sababu hiyo tuhudumiane kwa Upendo.
Wagalatia 5:13 “Maana ninyi, ndugu, mliitwa
mpate uhuru; lakini uhuru wenu usiwe sababu ya kuufuata mwili, bali tumikianeni
kwa upendo.”
Kila mwanafunzi wa shule ya
huduma anapaswa kufahamu kuwa ameitwa kwaajili ya kuwatia nguvu wengine,
kufarijiana, kujengana na kunoana, kumbuka kuwa chuma hunoa chuma!
1Wathesalonike 5:9-11. “Kwa kuwa Mungu
hakutuweka kwa hasira yake, bali tupate wokovu, kwa Bwana wetu Yesu Kristo;
ambaye alikufa kwa ajili yetu, ili tuishi pamoja naye, kwamba twakesha au
kwamba twalala. Basi, farijianeni na kujengana kila mtu na mwenzake, vile vile
kama mnavyofanya.”
Kila mwanafunzi wa shule ya
huduma anapaswa kufahamu kuwa anapaswa kusaidia huduma ya kichungaji, karama za
huduma tulizo nazo ni huduma za masaidiano kwa hiyo katika kanisa tunawasaidia
viongozi wetu katika kubeba maono, kulinda umoja na kusaidia kazi za kichungaji
Warumi 12:4-8 “Kwa kuwa kama vile katika
mwili mmoja tuna viungo vingi, wala viungo vyote havitendi kazi moja; Vivyo
hivyo na sisi tulio wengi tu mwili mmoja katika Kristo, na viungo, kila mmoja
kwa mwenzake. Basi kwa kuwa tuna karama zilizo mbalimbali, kwa kadiri ya neema
mliyopewa; ikiwa unabii, tutoe unabii kwa kadiri ya imani; ikiwa huduma, tuwemo
katika huduma yetu; mwenye kufundisha, katika kufundisha kwake; mwenye kuonya,
katika kuonya kwake; mwenye kukirimu, kwa moyo mweupe; mwenye kusimamia kwa bidii
mwenye kurehemu, kwa furaha.”
Na. Rev. Innocent Samuel Kamote.
Mkuu wa wajenzi
mwenye Hekima



