Jumapili, 18 Januari 2026

Walinichukia bure!


Zaburi 69:4 “Wanaonichukia bure ni wengi Kuliko nywele za kichwa changu. Watakao kunikatilia mbali wamekuwa hodari, Adui zangu kwa sababu isiyo kweli. Hata mimi nalilipishwa kwa nguvu Vitu nisivyovichukua.”

Yohana 15:24-25 “Kama nisingalitenda kwao kazi asizozitenda mtu mwingine, wasingalikuwa na dhambi; lakini sasa wametuona mimi na Baba yangu, na kutuchukia. Lakini litimie lile neno lililoandikwa katika torati yao, Walinichukia bure.”



Utangulizi:

Je umewahi kupitia hali katika maisha ambapo umekumbana na watu katika mazingira fulani kisha wakakuchukia tu bila ya sababu?  Au wakakupinga tu au wakakukataa, au ukakaliwa vikao, au kuitwa kwenye mabaraza ya watu waliojaa chuki na wivu wewe ukawa ndio agenda na kisha yakatolewa maamuzi ya kukuhukumu wewe hata bila ya sababu yenye mashiko? “Walinichukia bure bila ya sababu” ni moja ya usemi wenye nguvu sana wa kibiblia  ambao kivuli chake ni Zaburi 69:4 na Asili yake ni Yohana 15:24-25 ambapo Daudi pamoja na Yesu Kristo wanaelezea namna na jinsi walivyochukiwa na watu au maadui zao bila ya sababu, wakiwashambulia na kuwachukia  na kuwahukumu, na kuwapinga, na kuwafukuza bila sababu za haki, au kwa sababu ya chuki, wivu na kutokueleweka!, hata ingawa kuchukiwa, kukataliwa, kutokueleweka, na kuhukumiwa isivyo haki kunaweza kuwa na maumivu fulani kisaikolojia au kimwili, lakini kimaandiko jambo hili sio jipya kwani Biblia inatufundisha namna ya kuonyesha jinsi kupokea na kuonyesha mwitikio kwa mambo madogo kama haya kiroho  na sababu kwa nini unachukiwa bure bila sababu za maana, tutajifunza somo hili zuri Walinichukia bure! kwa kuzingatia vipengele vikuu muhimu vitatu vifuatavyo;-

·         Maana ya kuchukiwa bure!

·         Sababu za kuchukiwa bure

·         Jinsi ya kupokea na kuitikia chuki zao za bure


Maana ya kuchukiwa bure!

Yohana 15:24-25 “Kama nisingalitenda kwao kazi asizozitenda mtu mwingine, wasingalikuwa na dhambi; lakini sasa wametuona mimi na Baba yangu, na kutuchukia. Lakini litimie lile neno lililoandikwa katika torati yao, Walinichukia bure.”

Ni muhimu kufahamu kuwa neno kuchukiwa katika lugha ya Kiebrania linatumika neno śānē  ambalo maana yake kwa kiingereza ni to detest, oppose or treat as an enemy  kwa Kiyunani (Greek) ni miseō ambalo kwa kiingereza ni to detest, reject, persecute or love less intentionally  katika msamiati wa kisaikolojia linatumika neno “antipathy” ambalo kiingereza ni a strong feeling of dislike kwa hiyo kuchukiwa katika lugha ya Kiswahili kwa maana hizo hapo juu tunaweza kutafasiri kama Hisia kali za kutokukubali, hisia za kukukataa, hisia za kukupinga, hisia za kukuona kama adui, hisia za kutokukupenda, hisia za kutamani wakutese au upatwe na mabaya au usiwepo, au kuhisi kukuchukia tu bila sababu za maana za makusudi au za kutokukusudia chuki hii inasukumwa na wivu wa kiroho moyoni mwa watu kwa sababu ya kibali cha kiungu ndani yako, kwa hiyo chuki hii wakati mwingine inaweza kutoka kwa watu waliokuzidi kila kitu,  wana cheo, wana mali, wana elimu, wakati mwingine hata umri mkubwa kuliko wako lakini wakikuona tu wanakuchukia bila sababu na unaweza kujiuliza mbona mimi sina lolote kama wao lakini wanakuchukia tu, Daudi anasema walionichukia ni hodari  wanaotamani kumkatilia mbali wana nguvu lakini hata hivyo walimchukia bure tu, hii ni chuki ambayo asili yake ni mambo ya rohoni na wivu wenye uchungu!

Zaburi 69:4 “Wanaonichukia bure ni wengi Kuliko nywele za kichwa changu. Watakao kunikatilia mbali wamekuwa hodari, Adui zangu kwa sababu isiyo kweli. Hata mimi nalilipishwa kwa nguvu Vitu nisivyovichukua.”

Hapo tumeona maana ya neno chuki lakini vile vile neno “bure” katika biblia ya kiebrania linasomeka kama “hinnām” ambalo kwa kiingereza ni “unjustly” na katika biblia ya kiyunani linasomeka kama “dōrean” ambalo maana yake “undeservedly”  katika Kiswahili cha kimahakama kuchukiwa huku kulikuwa kusikokuwa na sababu za haki, kwa dhuluma, bila makosa ya kimahakama, bila kukutwa na hatia, isivyohalali, kwa hiyo watu wanaweza kukuchukia wewe kwa sababu isiyoweza kuthibitishwa kimahakama, kwamba mtuhumiwa ana makosa gani, kwa mfano Daudi alilipishwa kwa nguvu vitu ambavyo hakuvichukua, au Yesu alihukumiwa mahakamani huku hakimu akigundua kuwa ilikuwa ni wivu tu, walimtoa kwa husuda, hakuwa amewakosea wao, wala mtu yeyote.

Mathayo 27:17-18 “Basi walipokutanika, Pilato akawaambia, Mnataka niwafungulie yupi? Yule Baraba, au Yesu aitwaye Kristo? Kwa maana alijua ya kuwa wamemtoa kwa husuda.”

Unaona ndugu yangu unaweza kuchukiwa bure katika maisha haya ya kutembea na Yesu unaweza kupigwa vita, unaweza kuchukiwa bila ya sababu, unaweza kuchukiwa kwa sababu zisizo za kweli wala za haki, unaweza kuchukiwa hata na watu uliowahi kuwaomba msamaha hata pamoja na kuwa wamekukosea wao, chuki hii ni chuki ya husuda na haina mashiko, yanapokutokea haya katika maisha ya wokovu na wakati mwingine kutoka kwa watu waliookoka tena wenye nguvu kuliko wewe fahamu umebeba kusudi kubwa na maalumu, fahamu wewe ni mwanafunzi wa Yesu kweli kweli wala usifadhaike, Neno la Mungu linatufunulia siri hizo muhimu zinazopelekea wewe uchukiwe

Sababu za kuchukiwa bure.

Ni muhimu kufahamu kuwa chuki za bure kwako zinafunua maana pana sana za kiwango cha kiroho ulichokifikia, wakristo wengi leo wanaishi maisha ya kinafiki na sio wakweli kwa Mungu wala kwa wanadamu, wengi wanaishi maisha ya kuigiza, wanaonekana kama watu maarufu kwa nje, wakiwa na elimu kubwa, na vyeo vikubwa na wenye pesa na nguvu lakini hawana nguvu za kiroho walishakufa zamani na wamepoteza kabisa kujiamini, na kiroho wamefilisika, unapokuwa mwanafunzi wa kweli wa Yesu na mfuasi wa kweli wa Bwana Yesu katika karne hizi, watakupendea nini? Wakupende kwa lipi? Kama wewe ni mwana wa Mungu tu hawakupendi, kama hujawahi kuwafanya lolote tu wanakuchukia bure je wataweza kuwapenda adui wa kweli ambao Yesu amesema wapendeni adui zenu? Waombeeni wanaowaudhi?, huoni kuwa agizo hilo ni la juu zaidi? Wewe maisha yako yanawapa tabu, kama Yesu alivyowapa taabu mafarisayo na masadukayo, kwa hiyo unapoona wanakuchukia bure ziko sababu nyingi na hapa na ainanisha chache:-

1.       Kwa sababu wewe ni nuru – Mtu wa Mungu ni hivi unapoishi maisha ya nuruni, hapa maana yake wewe ni mkweli kwa Mungu, unapokosea unatubu, na unasonga mbele na huna kinyongo na mtu na Mungu yuko upande wako na anakutetea na kukupigania basi elewa hivi maisha yako ya nuruni yanalifanya giza lidhalilike, hata kama husemi lolote lakini kuishi kwako kwa haki hata bila ya maneno kunawafunua wenye dhambi, kwa hiyo watu wanaweza kukuchukia sio kwa sababu ya kitu umefanya bali kwa sababu kuna kitu unakiwakilisha

 

Yohana 3:19-21 “Na hii ndiyo hukumu; ya kuwa nuru imekuja ulimwenguni, na watu wakapenda giza kuliko nuru; kwa maana matendo yao yalikuwa maovu. Maana kila mtu atendaye mabaya huichukia nuru, wala haji kwenye nuru, matendo yake yasije yakakemewa. Bali yeye aitendaye kweli huja kwenye nuru, ili matendo yake yaonekane wazi ya kuwa yametendwa katika Mungu.”

 

1Yohana 2:9-11 “Yeye asemaye kwamba yumo nuruni, naye amchukia ndugu yake, yumo gizani hata sasa. Yeye ampendaye ndugu yake, akaa katika nuru, wala ndani yake hamna kikwazo. Bali yeye amchukiaye ndugu yake, yu katika giza, tena anakwenda katika giza, wala hajui aendako, kwa sababu giza imempofusha macho.”          

 

2.       Kwa sababu wewe si wa ulimwengu huu – Mtu wa Mungu kama wewe ni wa Yesu Kristo hivi unadhani ulimwengu utakupenda? Ukupende wewe nani? Ukupende wewe umeutendea nini? Ukupende wakati unafunua siri za Mungu? Ukupende wakati hata Yesu Mwenyewe walimchukia bure wewe kama u mwanafunzi wa Yesu utachukiwa tu, Yesu alisema kama mimi mwenyewe walinickukia mwanafunzi hampiti Mwalimu wake yaani kila mwanafunzi wa kweli wa Yesu atachukiwa tu, mpendwa chuki hiyo ni ushahidi wa wazi kwamba unamlingania Yesu Kristo, kuchukiwa kwako sio ushahidi wa kushindwa kwako bali ni ushahidi ya kuwa unamuishia Yesu Kristo  na sio hivyo tu hata mafundisho yetu yatakataliwa kama yalivyokataliwa ya Yesu

 

Yohana 15:18-20 “Iwapo ulimwengu ukiwachukia, mwajua ya kuwa umenichukia mimi kabla ya kuwachukia ninyi. Kama mngekuwa wa ulimwengu, ulimwengu ungewapenda walio wake; lakini kwa kuwa ninyi si wa ulimwengu, bali mimi naliwachagua katika ulimwengu, kwa sababu hiyo ulimwengu huwachukia. Likumbukeni lile neno nililowaambia, Mtumwa si mkubwa kuliko bwana wake. Ikiwa waliniudhi mimi, watawaudhi ninyi; ikiwa walilishika neno langu watalishika na lenu.”

 

3.       Kwa sababu wewe ni wa rohoni na wao ni wa mwilini – Mtu wa Mungu ninataka nikuambie ya kwamba ulimwengu tulio nao una makundi makuu mawili tu, haijalishi kundi hilo liko kanisani au nje lakini kokote kwenye watu kuna aina mbili za watu watu wa rohoni na watu wa mwilini, wale wa mwilini huwaudhi wale wa rohoni hii ni kanuni ya kibiblia iliyokuwako zamani na inatenda kazi hata sasa, kama wewe ni mzaliwa wa kiroho utaudhiwa na yule wa mwilini tu ona  

 

Wagalatia 4:29 “Lakini kama vile siku zile yule aliyezaliwa kwa mwili alivyomwudhi yule aliyezaliwa kwa Roho, ndivyo ilivyo na sasa.”

 

4.       Kwa sababu ya kibali cha Mungu juu yako – Ndugu yangu mpendwa kama Mungu amekupa kibali, Mungu amekupaka mafuta, Mungu ana matumizi na wewe Mungu ana kusudi na wewe kibali cha Mungu juu yako kinawanyanyasa kisaikolojia wale wasio na kibali hicho sasa wakuchekee? Wakutie moyo, wakukubali wakati wanatamani kusikia umeharibikiwa, wanatamani hata ufe leo, Daudi anasema wanaomchukia ni wengi kuliko nywele za kichwa chake, kaangalie mashariki ya kati Israel inapendwa? Wanatamani waifutilie mbali wanatamani waikatilie mbali ndivyo ulivyo na wewe mtu wa Mungu, kibali chako kinawasumbua haijalishi hali ya nje kuwa wao wana nguvu lakini upako wako unawanyanyasa ndio maana wanakuchukia bure

 

1Samuel 29:6-8 “Hata ikawa, walipokuwa wakienda, hapo Daudi aliporudi baada ya kumwua yule Mfilisti, wanawake wakatoka katika miji yote ya Israeli, kwa kuimba na kucheza, ili kumlaki mfalme Sauli; wakatoka na matari, na shangwe, na vinanda. Nao wale wanawake wakaitikiana wakicheza, wakasema, Sauli amewaua elfu zake, Na Daudi makumi elfu yake. Basi Sauli akaghadhibika sana, na maneno haya yakamchukiza; akasema, Wamempa Daudi makumi elfu, na mimi wamenipa elfu tu; kuna nini tena awezayo kupata, isipokuwa ni ufalme?

 

Mwanzo 37:3-11 “Basi Israeli akampenda Yusufu kuliko wanawe wote, maana ni mwana wa uzee wake, akamfanyia kanzu ndefu. Ndugu zake wakaona ya kuwa baba yao anampenda kuliko ndugu zake wote, wakamchukia, wala hawakuweza kusema naye kwa amani. Yusufu akaota ndoto, akawapa ndugu zake habari, nao wakazidi kumchukia; akawaambia, Tafadhalini, sikieni ndoto hii niliyoiota. Tazama, sisi tulikuwa tukifunga miganda shambani, kumbe! Mganda wangu ukaondoka ukasimama, na tazama, miganda yenu ikazunguka ikainama mbele ya mganda wangu. Ndugu zake wakamwambia, Je! Kweli wewe utatumiliki sisi? Nawe utatutawala sisi? Wakazidi kumchukia kwa ajili ya ndoto yake, na kwa maneno yake. Akaota tena ndoto nyingine, akawaambia ndugu zake, akasema, Angalieni, nimeota ndoto nyingine; na tazama, jua na mwezi na nyota kumi na moja zikaniinamia. Akawaambia baba yake na ndugu zake; baba yake akamkemea akamwambia, Ni ndoto gani hii uliyoiota? Je! Mimi na mama yako na ndugu zako tutakuja tukusujudie hata nchi? Ndugu zake wakamhusudu; bali baba yake akalihifadhi neno hili.”

 

5.       Kwa sababu ya wivu wenye uchungu – Mpendwa wakati mwingine wewe unachukiwa bure kwa sababu ya wivu, ni wivu tu, kuna kitu wakijilinganisha na wewe au na ninyi  wanakuona kabisa unakwenda mbele, wanakuona kabisa uko tofauti hata kama kwa sasa huna kitu wanakuona na wanajua uweza wa Mungu juu yako na kile ambacho Mungu amewekeza ndani yako wakupende kwa lipi wakati wamejaa wivu, wamejaa wivu huu ni wivu wenye uchungu wivu wa kujilinganisha na wao na wakijilinganisha na wewe wanaona kuna kitu cha ziada kwako wivu huu wa kujilinganisha unaitwa “phthonos” kwa kiingereza “is hatred rooted in comparison”  Yesu alichukiwa kwa sababu alikuwa na kitu cha ziada kuliko mafarisayo na masadukayo, kwa hiyo walikuwa na wivu uliojaa chuki aina hii ya wivu wakati mwingine huwazungumzia watu vibaya  na mambo mabaya ili wao waonekane wema yule mwema aonekane mbaya.

 

Mathayo 27:17-18 “Basi walipokutanika, Pilato akawaambia, Mnataka niwafungulie yupi? Yule Baraba, au Yesu aitwaye Kristo? Kwa maana alijua ya kuwa wamemtoa kwa husuda.”

 

Matendo 5:16-20 “Nayo makutano ya watu wa miji iliyoko kandokando ya Yerusalemu wakakutanika, wakileta wagonjwa, nao walioudhiwa na pepo wachafu; nao wote wakaponywa. Akaondoka Kuhani Mkuu na wote waliokuwa pamoja naye, (hao ndio walio wa madhehebu ya Masadukayo), wamejaa wivu, wakawakamata mitume wakawaweka ndani ya gereza; lakini malaika wa Bwana akafungua milango ya gereza usiku, akawatoa, akasema, Enendeni mkasimame hekaluni mkawaambie watu maneno yote ya Uzima huu.”

 

Waebrania 12:14-15. “Tafuteni kwa bidii kuwa na amani na watu wote, na huo utakatifu, ambao hapana mtu atakayemwona Bwana asipokuwa nao; mkiangalia sana mtu asiipungukie neema ya Mungu; shina la uchungu lisije likachipuka na kuwasumbua, na watu wengi wakatiwa unajisi kwa hilo.”    

 

6.       Kwa sababu ya vita vya kiroho – Wakati mwingine ile chuki inatokana na mapepo, kwa kadiri shetani alivyo adui yetu na anavyotuchukia sisi ndivyo anavyowatumia mapepo na maajenti wake au wakristo dhaifu kutumiwa na mapepo kutushambulia kwa hio wakati mwingine hii chuki kubwa unayoiona dhidi yako mtu wa Mungu ni ya shetani akiwatumia watu wake au vyombo vyake ili kupingana na kile ambacho Mungu amewekeza ndani yako

 

Waefeso 6:12 “Kwa maana kushindana kwetu sisi si juu ya damu na nyama; bali ni juu ya falme na mamlaka, juu ya wakuu wa giza hili, juu ya majeshi ya pepo wabaya katika ulimwengu wa roho.”

 

7.       Kwa sababu ya kuishi maisha ya utauwa -  kila unapokusudia na kuthubutu kuishi maisha ya tofauti na wengine maisha ya utakatifu na kuimarisha uhusiano wako wa siri na Mungu watu wabaya  na wadanganyaji wanaendelea kuteseka  na watakucukia, wewe jaribu kuishi na kuigiza kila alichikifanya bwana Yesu, jitoe kama yeye fuata mfano wake uone kama dunia itakupongeza hata kidogo!  Utachukiwa, utateswa, utadhihakiwa, utakataliwa, utaonekana huna faida, kwa sababu maisha ya kujitoa kwa Mungu yanapingana nay a dunia hii, viwango vya kuishi kama Kristo vinawaudhi wahuni,  vinawapa changamoto na kuwafanya wote walio vufuvugu na wasiookoka  wakose Amani, kwa hiyo kuchukiwa ni sehemu ya gharama za uaminifu wako kwa Mungu au kumfuata Yesu kwa uaminifu

 

2Timotheo 3:12-15 “Naam, na wote wapendao kuishi maisha ya utauwa katika Kristo Yesu wataudhiwa. lakini watu wabaya na wadanganyaji wataendelea, na kuzidi kuwa waovu, wakidanganya na kudanganyika. Bali wewe ukae katika mambo yale uliyofundishwa na kuhakikishwa, kwa maana unajua ni akina nani ambao ulijifunza kwao; na ya kuwa tangu utoto umeyajua maandiko matakatifu, ambayo yaweza kukuhekimisha hata upate wokovu kwa imani iliyo katika Kristo Yesu.”   

 

Jinsi ya kupokea na kuitikia chuki zao za bure

Ni jambo la kumshukuru Mungu kwamba Mungu ametupa akili na ufahamu katika neno lake namna na jinsi ya kushughulika na watu wanaotuchukia na njia hizo ni njia za kiroho, ambazo kimsingi zitakufanya wewe kuzidi bali adui zako kupungua, njia hizi ukizitumia zitakamilisha uwezo wako wa kiroho na kukunoa na kukufanya wewe uendelee kukua kiroho zaidi na kumfanania baba wa mbinguni

1.       Kunyamaza kimya – Moja ya njia ya kiroho ambayo Yesu Kristo aliitumia pale waliokuwa wakimchukia walipokuwa wakimsingizia mambo ya uongo ambayo hayana ukweli wowote bali kwa lengo la kumchafua na kuharibu tu wito wake yeye alikaa kimya, alipoonewa aikaa kimya alipoteswa na kutukanwa alikaa kimya, Neno kukaa kimya katika kiyunani ni “loidoreō kwa kiingereza ni “revile” ambalo maana yake ni “to insult verbally” hakutumia lugha chafu kujibu alinyamaza kimya badala ya kujibu “silence over revenge”  na alijikabidhi kwa Mungu ahukumuye kwa haki, Mpendwa mwachie Mungu atajibu kwa haki, Mungu huwapigania watu wakimya

 

1Petro 2:21-23 “Kwa sababu ndio mlioitiwa; maana Kristo naye aliteswa kwa ajili yenu, akawaachia kielelezo, mfuate nyayo zake.Yeye hakutenda dhambi, wala hila haikuonekana kinywani mwake. Yeye alipotukanwa, hakurudisha matukano; alipoteswa, hakuogofya; bali alijikabidhi kwake yeye ahukumuye kwa haki.”

 

Isaya 53:7 “Alionewa, lakini alinyenyekea, Wala hakufunua kinywa chake; Kama mwana-kondoo apelekwaye machinjoni, Na kama vile kondoo anyamazavyo Mbele yao wakatao manyoya yake; Naam, hakufunua kinywa chake.”

 

Hesabu 12:1-9 “Kisha Miriamu na Haruni wakamnenea Musa kwa sababu ya mwanamke Mkushi aliyekuwa amemwoa; maana, alikuwa amemwoa mwanamke Mkushi. Wakasema, Je! Ni kweli Bwana amenena na Musa tu? Hakunena na sisi pia? Bwana akasikia maneno yao. Basi huyo mtu, huyo Musa, alikuwa mpole sana zaidi ya wanadamu wote waliokuwa juu ya uso wa nchi. Bwana akanena ghafula na Musa, na Haruni na Miriamu, na kuwaambia, Tokeni nje ninyi watatu, mwende hemani mwa kukutania. Basi hao watatu wakatoka nje. Bwana akashuka katika nguzo ya wingu akasimama pale mlangoni pa Hema, akawaita Haruni na Miriamu, nao wakatoka nje wote wawili. Kisha akawaambia, Sikizeni basi maneno yangu; Akiwapo nabii kati yenu, Mimi, Bwana, nitajifunua kwake katika maono, Nitasema naye katika ndoto. Sivyo ilivyo kwa mtumishi wangu, Musa; Yeye ni mwaminifu katika nyumba yangu yote; Kwake nitanena mdomo kwa mdomo, Maana, waziwazi wala si kwa mafumbo; Na umbo la Bwana yeye ataliona. Mbona basi ninyi hamkuogopa Kumnenea mtumishi wangu, huyo Musa? Hasira za Bwana zikawaka juu yao; naye akaenda zake.”

 

2.       Waombee wanao kuudhi – Maandiko yanatufundisha kutoka mafundisho na maendo ya Bwana wetu Yesu na watakatifu walioyutangulia kuwa kuna haja ya kuwaombea wale wanaotuchukia, tuwaonee huruma na tuwapende kwa sababu wao ni dhaifu

 

Mathayo 5:43-45 “Mmesikia kwamba imenenwa, Umpende jirani yako, na, Umchukie adui yako; lakini mimi nawaambia, Wapendeni adui zenu, waombeeni wanaowaudhi, ili mpate kuwa wana wa Baba yenu aliye mbinguni; maana yeye huwaangazia jua lake waovu na wema, huwanyeshea mvua wenye haki na wasio haki.”

 

Luka 23:33-34 “Na walipofika mahali paitwapo Fuvu la Kichwa, ndipo walipomsulibisha yeye, na wale wahalifu, mmoja upande wa kuume, na mmoja upande wa kushoto. Yesu akasema, Baba, uwasamehe, kwa kuwa hawajui watendalo. Wakagawa mavazi yake, wakipiga kura.”

 

3.       Endelea kutenda mema -  Lengo kubwa la shetani wakati mwingine kukushambulia kupitia watu ni ili wewe uwe mtu mbaya, uone kuwa kila unapotenda mema unalipwa mabaya kwa hiyo unaamua kufunga milango yako ya wema na kuwa mbinafsi lakini neno la Mungu linatutaka tuendelee kuwa washindi kwa kutenda mema, kadiri unavyoendelea kuwa mwema na kutenda haki wema wako utawanyamazisha maadui zako na kila ubaya wanaokuzushia

 

Warumi 12:19 “Wapenzi, msijilipize kisasi, bali ipisheni ghadhabu ya Mungu; maana imeandikwa, Kisasi ni juu yangu mimi; mimi nitalipa, anena Bwana.Lakini, Adui yako akiwa na njaa, mlishe; akiwa na kiu, mnyweshe; maana ufanyapo hivyo, utampalia makaa ya moto kichwani pake. Usishindwe na ubaya, bali uushinde ubaya kwa wema.”

 

4.       Endelea kupiga kazi, endelea kumtumikia Mungu – Wakati maadui zako wanapokushambulia wewe ongezea viwango vya kumtumikia Mungu na kufanya kazi kwa bidii, kadiri unavyoendelea kumtumikia Mungu kwa bidii Mungu ataendelea kukubariki na kazi unazozifanya zitatangaza kile kitu Mungu ameweka ndani yako,  na kuudhihirishia ulimwengu kuwa yeye yuko na wewe, unapoendelea kumtumikia Mungu kwa nguvu Baraka zako zinaendelea kuongezeka na adui zako wanaendelea kuwekwa uchi neno la Mungu linasema adui zako watakuonyesha maungo yao, yaani uchi zao zitafunuliwa, aibu zao zitawekwa wazi, utupu wao utahukumiwa na kazi unazozifanya wataaibika na kazi yako itasema si biblia imesema kwa matunda yao mtawatambua, je mti mbaya unaweza kuzaa matunda mema?

 

Kutoka 23:25-27 “Nanyi mtamtumikia BWANA, Mungu wenu, naye atakibarikia chakula chako, na maji yako; nami nitakuondolea ugonjwa kati yako. Hapatakuwa na mwenye kuharibu mimba, wala aliye tasa, katika nchi yako; na hesabu ya siku zako nitaitimiza.Nitatuma utisho wangu utangulie mbele yako, nami nitawafadhaisha watu wote utakaowafikilia, nami nitawafanya hao adui zako wote wakuonyeshe maungo yao.”   

 

Yohana 10:37-38 “Kama sizitendi kazi za Baba yangu, msiniamini; lakini nikizitenda, ijapokuwa hamniamini mimi, ziaminini zile kazi; mpate kujua na kufahamu ya kuwa Baba yu ndani yangu, nami ni ndani ya Baba.”

 

Chuki kutoka kwa wapendwa na watumishi wenzako haimaanishi kuwa Mungu amekuacha bali inakufundisha kuelewa maswala ya kiroho, sio kuwa wakati wote watu watakuchukia kwa sababu wewe ni muovu hapana bali kwa sababu wao ni dhaifu kiroho, Mungu anakufundisha uwezo wa kuvumilia kabla ya kukuinua kukubariki na kukutumia, Mungu anakufundisha kuwa kama Yeye, wewe hujasahaulika, wewe hujashindwa wewe uko sawa na Daudi, uko sawa na Yusufu unafafanana na Yesu  na  ndio maana unachukiwa bila ya sababu za halali, wewe utakuwa kiroho vizuri zaidi, ukiyamudu hayo machungu yote ujue wazi kuwa thawabu yako ni kubwa sana mbinguni


Mathayo 5:11-12 “Heri ninyi watakapowashutumu na kuwaudhi na kuwanenea kila neno baya kwa uongo, kwa ajili yangu. Furahini, na kushangilia; kwa kuwa thawabu yenu ni kubwa mbinguni; kwa maana ndivyo walivyowaudhi manabii waliokuwa kabla yenu.”              

 

Na. Rev. Innocent Samuel Kamote


Mkuu wa wajenzi mwenye Hekima.

Jumapili, 11 Januari 2026

Mwanzi uliopondeka hatauvunja!


Isaya 42:1-4 “Tazama mtumishi wangu nimtegemezaye; mteule wangu, ambaye nafsi yangu imependezwa naye; nimetia roho yangu juu yake; naye atawatolea mataifa hukumu. Hatalia, wala hatapaza sauti yake, wala kuifanya isikiwe katika njia kuu. Mwanzi uliopondeka hatauvunja, wala utambi utokao moshi hatauzima; atatokeza hukumu kwa kweli. Hatazimia, wala hatakata tamaa, hata atakapoweka hukumu duniani; na visiwa vitaingojea sheria yake.”



Utangulizi:

Kaka zangu na dada zangu katika Bwana, Leo tutachukua muda kujifunza mojawapo ya unabii wa muhimu sana katika huduma ya Masihi ambao kimsingi ulikuja kutimizwa katika agano jipya, Wakati wa huduma ya Masihi hapa duniani, Unabii huu ambao kimsingi unatufundisha kusudi kubwa la huduma na moyo wa Masihi Yesu Kristo hapa ulimwenguni, jinsi alivyojawa na huduma iliyojaa rehema na upendo unaopitiliza mipaka ya kawaida ya huduma za kibinadamu na kidini.

Mathayo 12:15-21 “Naye Yesu hali akiyafahamu hayo akaondoka huko; na watu wengi wakamfuata; akawaponya wote, akawakataza wasimdhihirishe; ili litimie neno lililonenwa na nabii Isaya, akisema, Tazama, mtumishi wangu niliyemteua; Mpendwa wangu, moyo wangu uliyependezwa naye; Nitatia roho yangu juu yake, Naye atawatangazia Mataifa hukumu. Hatateta wala hatapaza sauti yake; Wala mtu hatasikia sauti yake njiani. Mwanzi uliopondeka hatauvunja, Wala utambi utokao moshi hatauzima, Hata ailetapo hukumu ikashinda. Na jina lake Mataifa watalitumainia.”

Kwa ujumla unabii wa Isaya na kutimia kwake kunatukumbusha jambo muhimu sana na lenye kutia moyo ya kuwa Ufalme wa Mungu unatenda kazi katika msingi wa rehema, urejesho na huruma zisizotikisika! “Mwanzi uliopondeka hatauvunja na utambi utokao moshi hatauzima” vinawakilisha nini hasa katika ujumbe huu? Bila shaka Mungu Roho Mtakatifu atatupa kuelewa; Tutajifunza somo hili Mwanzi uliopondeka hatauvunja kwa kuzingatia vipengele vikuu vitatu vifuatavyo:-

·         Ufahamu kuhusu mwanzi uliopondeka na utambi utokao moshi

·         Huduma ya kimasihi mwanzi uliopondeka na utambi utokao moshi

·         Mwanzi uliopondeka na utambi utokao moshi


Ufahamu kuhusu mwanzi uliopondeka na utambi utokao moshi.

Ni muhimu kufahamu kuwa usemi wa “mwanzi uliopondeka na utambi utoka moshi” ni usemi wenye maana gani kinabii kabla ya kuunganisha na kuangalia huduma ya kimasihi itakavyokuwa, Neno mwanzi linalotumika katika maandiko ya kiingereza linatumika neno “REEDS” ambalo kwa Kiswahili maana yake ni nyasi, Hata hivyo nyasi ziko za aina mbalimbali, kwa hiyo nyasi hizi katika

lugha ya Kiebrania zinaitwa kwa kutumia neno Kāneh kwa lugha ya Kilatini na Kiyunani linatumika neno Canna kwa kiingereza Cane  mmea huu kwa kawaida ulistawi sana pembeni mwa mto Jordan katika taifa la Israel kwa Kiswahili unaitwa MWANZI, majani ya Mwanzi au Cane kwa Kiyunani yanajulikana kama kálamos au Calamus, kwa Kiswahili Kalamu. Nyakati za agano la kale kabla ya kuwepo kwa teknolojia ya uandishi tuliyo nayo sasa Manabii na waandishi walitumia majani ya muanzi kama kalamu ya kuandikia, waliyatumia majani haya na kuchovya kwenye wino na kuyatumia kuandikia katika karatasi maalumu za nyakati hizo (Papyrus) au Magombo ya chuo ya ngozi, walichovya katika bakuli la wino kwa kutumia majani hayo yaliyoitwa kalamu na kisha kuyatumia kuandikia endapo kalamu ingechoka au kupondeka waliitupa na kuchomoa jani lingine la muanzi yaani kalamu na kutoka kwenye kitita cha majani hayo na kulitumia kuandika, waandishi wangeifanya kazi hiyo ngumu kutwa nzima na usiku, huku usiku wakitumia taa ya kibatali iliyotumia mafuta na utambi, manabii na waandishi walifanya kazi ya kuandika mpaka mafuta yangewaishia na taa ikazimika na utambi ungebaki unafuka moshi hapo wangezima kabisa na kulala wakiwa wamechoka sana kitendo cha kuvunjika kwa Kalamu au kuisha kwa utambi kulikwamisha kwa kiwango kikubwa kazi nzima ya uandishi, wakati huu nabii Isaya alipokea ujumbe wa kinabii kwamba kazi hiyo ya kuchosha itakuwa nyepesi, wakati wa Masihi, na wakati wa Masihi kalamu haitavunjika wala utambi hautaisha na kufuka moshi, uwepo wake utasababisha uzima katika mazingira yote.

Isaya 42:1-3 “Tazama mtumishi wangu nimtegemezaye; mteule wangu, ambaye nafsi yangu imependezwa naye; nimetia roho yangu juu yake; naye atawatolea mataifa hukumu. Hatalia, wala hatapaza sauti yake, wala kuifanya isikiwe katika njia kuu. Mwanzi uliopondeka hatauvunja, wala utambi utokao moshi hatauzima; atatokeza hukumu kwa kweli.”

Huduma ya kimasihi mwanzi uliopondeka na utambi utokao moshi

Kimsingi Mwanzi uliopondeka na utambi unaofuka moshi ulikuwa ni usemi uliotumika kuelezea pia kitu ambacho kimepoteza maana, hakifai tena kwa matumizi, kitu kinachokwamisha kazi ya uandishi kusonga mbele, lakini sio hivyo tu usemi huu ulitumika pia kuwaita mataifa mengine wasio wayahudi yaani mataifa, hao waliitwa pia mwanzi uliopondeka, na utambi utokao moshi ulimaanisha watu wa Mungu ambao wamepoteza thamani yao, yaani walikuwa Nuru na sasa wamezimika hawafai tena kwa matumizi, Mwanzi mataifa wasiofaa, Utambi wayahudi waliopoa.

Mwanzi uliopondeka – Uliwakilisha mataifa au watu wenye dhambi lakini pia, walemavu au wagonjwa, watu wasio na matumaini, waliokandamizwa ambao kila kitu kwao kimepoteza maana wamepoteza maana katika jamii, hawafai, wamevunjika, hawana matumizi tena, ni wa kutupwa, wanyonge, waliochoka nafsi zao, sababu ya changamoto, wenye laana, wenye mikosi wasioofaa kitu, wasio na uhakika wa wokovu, wanaohesabika kuwa sio kitu wanaosubiria kuchomwa moto.

Utambi utokao moshi – Uliwakilisha watu wa Mungu Israel wenyewe waliokuwa nuru lakini wamepoteza thamani wamepoa wamerudi nyuma, hawana thamani tena ni watenda dhambi wamepoa, wote wanaosubiria hukumu yao tu hawana kitu cha ziada zaidi ya kukwamisha kazi.

Isaya anaona kuwa wanasubiri maamuzi ya hakimu ambaye ni Masihi, yeye anajua atawahukumuje hiki ndicho Isaya alichokuwa anakiona katika unabii wake lakini anaona kama Masihi atakapokuja huenda mambo yatakuwa tofauti, kwani hukumu zake ni tofauti na uweza wake ni tofauti yeye Mwanzi uliopondeka hatauvunja, wala utambi utokao moshi hatauzima kwa kuwa yeye ana Roho wa Mungu, anapendezwa na Mungu anajua atayatimiza vipi mapenzi ya Mungu, Kwa Masihi hakutakuwa na mtu asiye na faida, hakutakuwa na mtu wa kutupwa, au kuzimwa ni wakati wa uamsho mkubwa sana Masihi atatenda kwa namna ya tofauti sana na mitazamo ya dini ya Kiyahudi

Huyu mataifa wanamtumainia, Kimsingi Isaya aliyatabiri maswala hayo katika unabii wake na Kristo Yesu alipokuja Duniani aliyatimiza haya na ndio Mathayo alipoyaona alikumbuka kile alichokuwa amekitabiri nabii Isaya akaandika sawa na unabii wa Isaya

Mathayo 12:15-21 “Naye Yesu hali akiyafahamu hayo akaondoka huko; na watu wengi wakamfuata; akawaponya wote, akawakataza wasimdhihirishe; ili litimie neno lililonenwa na nabii Isaya, akisema, Tazama, mtumishi wangu niliyemteua; Mpendwa wangu, moyo wangu uliyependezwa naye; Nitatia roho yangu juu yake, Naye atawatangazia Mataifa hukumu. Hatateta wala hatapaza sauti yake; Wala mtu hatasikia sauti yake njiani. Mwanzi uliopondeka hatauvunja, Wala utambi utokao moshi hatauzima, Hata ailetapo hukumu ikashinda. Na jina lake Mataifa watalitumainia.”

Masihi alipokuja alihukumu kwa haki kwani kwanza aliwaona wote kuwa ni wenye dhambi, Mataifa na Wayahudi pia na hakukuwa na aliye bora kuliko mwingine wote wanahitaji msaada wake, Wayahudi na Mataifa mengine wote ni wenye dhambi wote wanamuhitaji Masihi hakuna mwenye haki hata mmoja wala hakuna anayemtafuta Mungu wala hakuna anayetenda mema hata mmoja wala hakuna anayemcha Mungu, hakuna aliye bora kuliko mwingine hakuna mwenye nafuu wote wanahitaji rehema za Mungu na Masihi amekuja kwaajili hiyo hakuja kuhukumu amaekuja kutangaza rehema za Mungu, amekuja kutangaza msamaha wa dhambi, fadhili za Mungu na kuponya mwili na roho

Warumi 3:9-18 “Ni nini basi? Tu bora kuliko wengine? La! Hata kidogo. Kwa maana tumekwisha kuwashitaki Wayahudi na Wayunani ya kwamba pia wamekuwa chini ya dhambi; kama ilivyoandikwa, ya kwamba, Hakuna mwenye haki hata mmoja. Hakuna afahamuye; Hakuna amtafutaye Mungu. Wote wamepotoka, wameoza wote pia; Hakuna mtenda mema, la! Hata mmoja. Koo lao ni kaburi wazi, Kwa ndimi zao wametumia hila. Sumu ya fira i chini ya midomo yao. Vinywa vyao vimejaa laana na uchungu. Miguu yao ina mbio kumwaga damu. Uharibifu na mashaka yamo njiani mwao. Wala njia ya amani hawakuijua. Kumcha Mungu hakupo machoni pao.”

Huduma ya Masihi inatoa rehema kwa wote waliovunjika na waliopoa wanaofuka moshi tu lakini moto umezimika wote wanamuhitaji Yesu, achochee utambi uwake na aponye waliovunjika,  uvumilivu na upole na upendo wa Bwana wetu Yesu Kristo ndio unaowavumilia watu leo na kuwapa nafasi ili waponywe na moto uwake tena, lakini sio hivyo tu Yesu yuko tayari kushughulika na wote walioumizwa, wanaohitaji rehema na upendo wake yeye yuko tayari kuwahudumia na kuwaponya watu wote wanapaswa kumuendea na watu wote wanapaswa kulitegemea jina lake, Yeye hazimii wala hakati tamaa na mtu, watu wote watamtumainia na kuliitia jina lake yeye yuko tayari kusaidia.

Matendo 4:10-12 “jueni ninyi nyote na watu wote wa Israeli ya kuwa kwa jina la Yesu Kristo wa Nazareti, ambaye ninyi mlimsulibisha, na Mungu akamfufua katika wafu, kwa jina hilo mtu huyu anasimama ali mzima mbele yenu. Yeye ndiye jiwe lile lililodharauliwa na ninyi waashi, nalo limewekwa kuwa jiwe kuu la pembeni. Wala hakuna wokovu katika mwingine awaye yote, kwa maana hapana jina jingine chini ya mbingu walilopewa wanadamu litupasalo sisi kuokolewa kwalo.”                 

Mwanzi uliopondeka na utambi utokao moshi.

Mathayo 12:15-21 “Naye Yesu hali akiyafahamu hayo akaondoka huko; na watu wengi wakamfuata; akawaponya wote, akawakataza wasimdhihirishe; ili litimie neno lililonenwa na nabii Isaya, akisema, Tazama, mtumishi wangu niliyemteua; Mpendwa wangu, moyo wangu uliyependezwa naye; Nitatia roho yangu juu yake, Naye atawatangazia Mataifa hukumu. Hatateta wala hatapaza sauti yake; Wala mtu hatasikia sauti yake njiani. Mwanzi uliopondeka hatauvunja, Wala utambi utokao moshi hatauzima, Hata ailetapo hukumu ikashinda. Na jina lake Mataifa watalitumainia.”

Mathayo alipokuwa anawaona watu mbalimbali matajiri kwa masikini, wenye nguvu na wasio na nguvu wakimiminika kwa kutafuta msaada kwa Yesu alikumbuka kutimia kwa unabii wa Isaya na anaunukuu.

Huduma ya Masihi ilikazia ukweli kuwa Yesu hakuja kwaajili ya wenye nguvu, wala wenye kujitosheleza, wanaojifikiria kuwa wao ni wakamilifu amekuja kwaajlii ya waliovunjika wasio na faida waliozimika, Yesu alitakasa wenye ukoma, aliwagusa wakoma waliokuwa wamekataliwa, alisamehe wenye dhambi, aliwarejesha hata wale waliomkana mara tatu kama Petro, alishughulika na wale ambao wangestahili kubadilishwa na kutupwa, Mwanzi uliovunjika haukufaa tenza kwa waandishi zaidi ya kuchomwa moto na kutumia mwingine na utambi uliofuka moshi ulisubiri kubadilishwa, Lakini Masihi yeye angehuisha vile vinavyoonekana kutokufaa viweze kufaa kwa utukufu wa Mungu

Luka 5:30-32 “Ikawa Mafarisayo na waandishi wao kuwanung'unikia wanafunzi wake, wakisema, Mbona mnakula na kunywa pamoja na watoza ushuru na wenye dhambi? Yesu akajibu akawaambia, Wenye afya hawana haja na tabibu, isipokuwa walio hawawezi. Sikuja kuwaita wenye haki, bali wenye dhambi, wapate kutubu.”

Marko 16:6-7 “Naye akawaambia, Msistaajabu; mnamtafuta Yesu Mnazareti, aliyesulibiwa; amefufuka; hayupo hapa; patazameni mahali walipomweka. Lakini enendeni zenu, mkawaambie wanafunzi wake, na Petro, ya kwamba awatangulia kwenda Galilaya; huko mtamwona, kama alivyowaambia.”             

Yohana 21:15-17 “Basi walipokwisha kula, Yesu akamwambia Simoni Petro, Je! Simoni wa Yohana, wewe wanipenda kuliko hawa? Akamwambia, Naam ,Bwana, wewe wajua kuwa nakupenda. Akamwambia, Lisha wana-kondoo wangu. Akamwambia tena mara ya pili, Simoni wa Yohana, wanipenda? Akamwambia, Ndiyo, Bwana, wewe wajua kuwa nakupenda. Akamwambia, Chunga kondoo zangu. Akamwambia mara ya tatu, Simoni wa Yohana, wanipenda? Petro alihuzunika kwa vile alivyomwambia mara ya tatu, Wanipenda? Akamwambia, Bwana, wewe wajua yote; wewe umetambua ya kuwa nakupenda. Yesu akamwambia, Lisha kondoo zangu.”

Huduma ya kimasihi ni huduma ya uponyaji wa mwili nafsi na roho, ni huduma ya uvumilivu ni huduma ya huruma na upendo ni huduma ya kuchukuliana  na ni huduma ambayo haioni mkamilifu inaona kuwa kila mtu anahitaji huduma yake isipokuwa wale wenye kiburi tu na wale wanaojihesabia haki, kila mtu na kila mmoja anamuhitaji Bwana Yesu na ukarabati wa watu wa Mungu wa aina zote unatakiwa kupatikana kanisani, kanisani sio mahali pa watakatifu tu ni mahali pa watu wote wenye nguvu na dhaifu atakayekuja kuchuja ni Yesu mwenyewe, wajibu wetu sisi ni kuhubiri injili, na kuwafundisha watu na Neno la Mungu lenyewe litawabadilisha, Yesu mwenyewe atawaokoa na kuwasamehe watu wake yeye ndiye anayeweza kuwafinyanga watu wake wakawa kama yeye alivyo, hukumu halali itatolewa siku ya mwisho na mwenyewe sio sisi

Mathayo 13:47-50 “Tena ufalme wa mbinguni umefanana na juya, lililotupwa baharini, likakusanya samaki wa kila namna; hata lilipojaa, walilivuta pwani; wakaketi, wakakusanya walio wema vyomboni, bali walio wabaya wakawatupa. Ndivyo itakavyokuwa katika mwisho wa dunia; malaika watatokea, watawatenga waovu mbali na wenye haki, na kuwatupa katika tanuru ya moto; ndiko kutakuwako kilio na kusaga meno.”

Uko uwezekano kuwa unaona ujumbe huu huku ukiwa umevunjika moyo, una ndoa iliyovunjika, una uchumba uliovunjika una mahusiano yaliyopondeka, una nuru iliyozimika una hasara katika biashara na hujui utainukaje, una madeni, au utambi wako wa rohoni umezimika, matumaini ya maisha yako na ndoto zako zimekwama mahali.  Giza limetanda na kila kitu kinaonekana kukwama katika maisha yako, uwezo wako wa kusimama tena umepotea, muda wako umepotea, unajiuliza itakuwaje tena katika maisha yangu? Itakuwaje katika roho yangu? Je naweza kusimama tena hata baada ya kuharibu namna hii? Lakini kwa uwezo wa Bwana wetu Yesu Kristo, yeye anakuganga na kukuponya na kukuinua tena nakuhakikishia moto uliozimika utawaka na moyo uliovunjika utainuka hii ndio kazi ya Masihi amka leo acha kulia katika jina la Yesu Kristo mwana wa Mungu aliye hai, Yesu alikuja kwaajili ya watu kama wewe watu ambao wanatarajiwa kutupwa, na wanaoonekana kutokufaa katika jamii wenye matumaini yaliyofifia yeye haogopi hayo na anatoa mwaliko kuwa watu wote wenye changamoto zozote zile waje kwake

Mathayo 11:28-29 “Njoni kwangu, ninyi nyote msumbukao na wenye kulemewa na mizigo, nami nitawapumzisha. Jitieni nira yangu, mjifunze kwangu; kwa kuwa mimi ni mpole na mnyenyekevu wa moyo; nanyi mtapata raha nafsini mwenu;”

“Maombi yangu yafike kwako Moyo, uliopondeka hutadharau, Kiu yangu na haja yangu, nifanane nawe nifanane nawe, nifanane nawe, Nifanye kama wewe, unifinyange, nifinyange, wakinitazama wakuone wewe unifinyange, nifinyange”

Na. Rev. Innocent Samuel Kamote

Mkuu wa wajenzi mwenye Hekima!

Jumapili, 4 Januari 2026

Kuzingirwa kwa ukigo usioonekana!

 

Ayubu 1:7-9 “Bwana akamwuliza Shetani, Umetoka wapi wewe? Ndipo Shetani akamjibu Bwana, na kusema, Natoka katika kuzunguka-zunguka duniani, na katika kutembea huku na huku humo. Kisha Bwana akamwuliza Shetani, Je! Umemwangalia huyo mtumishi wangu Ayubu? Kwa kuwa hapana mmoja aliye kama yeye duniani, mtu mkamilifu na mwelekevu, mwenye kumcha Mungu na kuepukana na uovu. Ndipo Shetani akamjibu Bwana, na kusema, Je! Huyo Ayubu yuamcha Bwana bure? Wewe hukumzingira kwa ukigo pande zote, pamoja na nyumba yake, na vitu vyote alivyo navyo? Kazi za mikono yake umezibarikia, nayo mali yake imeongezeka katika nchi.”



Utangulizi:

Leo tunalenga kujifunza au kujikumbusha juu ya ulinzi wa Mungu usioonekana kwa watu wanaomwamini Mungu, katika kifungu cha maandiko ya msingi tunafunuliwa moja ya jambo la msingi lililoko katika ulimwengu wa roho ambalo macho yetu hayawezi kuona na huu ni ulinzi wa Mungu kupitia Malaika, Ukuta wa moto, Ukuta wa shaba, na wigo au ukigo usioonekana ambao kimsingi unawekwa na Mungu mwenyewe kwa watu wake, siri hii ya ukigo wa ulinzi uliowekwa na Mungu inafunuliwa na Shetani mwenyewe ambaye anakiri kuwa alikuwa hawezi kumshambulia Ayubu kwa sababu Mungu alikuwa amemuwekea ukigo pande zote, pamoja na nyumba yake, na vitu vyote alivyo navyo, ulinzi huu wa Mungu ni ulinzi usioonekana, ni ulinzi wa kiroho unaotokana na uhusiano wetu na Mungu na ni ulinzi unaowekwa na Mungu mwenyewe katika ulimwenguwa roho.

Zekaria 2:5 “Kwa maana mimi, asema Bwana, nitakuwa ukuta wa moto kuuzunguka pande zote, nami nitakuwa huo utukufu ndani yake.”

Yeremia 15:20-21 “Nami nitakufanya kuwa kama ukuta wa boma la shaba juu ya watu hawa; nao watapigana nawe; lakini hawatakushinda; maana mimi nipo pamoja nawe, ili nikuokoe, na kukuponya, asema Bwana. Nami nitakuokoa na mkono wa watu wabaya, nami nitakukomboa katika mkono wao wenye kutisha.”

Kwa msingi huo leo, tutachukua muda kujifunza somo hili Kuzingirwa kwa ukigo usioonekana kwa kuzingatia vipengele vikuu vitatu vifuatavyo:-

·         Maana ya ukigo usioonekana.

·         Kuzingirwa kwa ukigo usioonekana.

·         Jinsi ya kuzingirwa na ukigo usioonekana.


Maana ya ukigo usioonekana.

Siri ya kwamba watu wanaomcha Mungu wanazingirwa na ukigo pande zote inawekwa wazi kwa mara ya kwanza na Shetani mwenyewe wakati wa mazungumzo yake na Mungu katika ulimwengu wa roho kuhusu Mtumishi wa Mungu Ayubu aliyekuwako huku Duniani, Shetani katika mazungumzo yake na Mungu anaonekana kumjua vema Ayubu, kwa sababu hakuuliza ni Ayubu yupi? Na tena inaonekana wazi alikuwa anafahamu Ayubu anaishi wapi? Alikuwa anamfahamu Ayubu vizuri nje ndani na bila shaka alikuwa anafahamu kuwa Ayubu ni Mtumishi wa Mungu ambaye alikuwa mwaminifu kama maandiko yasemavyo, habari hii inatufunulia kwa kina kuwa kuna uwezekano wasaidizi wa shetani yaani mapepo na wenye mamlaka na wakuu wa giza kwa namna Fulani wamewahi kuwa na mpango mkakati wa kumshambulia Ayubu na huenda walishindwa, na walitoa taarifa kwa bwana wao kuwa Yule Bwana hawezekani analindwa na nguvu za Mungu, na inawezekana hatimaye hata Shetani mwenyewe alijaribu kumtembelea Ayubu na kujaribu kutaka kusababisha uharibifu lakini mbinu zilishindikana, ilibainika wazi kuwa Ayubu anazingirwa na ulinzi maalumu wa Mungu, na kila anachikifanya Mungu amekibariki.       

Ayubu 1:7-9 “Bwana akamwuliza Shetani, Umetoka wapi wewe? Ndipo Shetani akamjibu Bwana, na kusema, Natoka katika kuzunguka-zunguka duniani, na katika kutembea huku na huku humo. Kisha Bwana akamwuliza Shetani, Je! Umemwangalia huyo mtumishi wangu Ayubu? Kwa kuwa hapana mmoja aliye kama yeye duniani, mtu mkamilifu na mwelekevu, mwenye kumcha Mungu na kuepukana na uovu. Ndipo Shetani akamjibu Bwana, na kusema, Je! Huyo Ayubu yuamcha Bwana bure? Wewe hukumzingira kwa ukigo pande zote, pamoja na nyumba yake, na vitu vyote alivyo navyo? Kazi za mikono yake umezibarikia, nayo mali yake imeongezeka katika nchi.”

Tunafunuliwa hapo kuwa ulinzi huu wa Mungu ambao hapo unatajwa kama UKIGO sio ulinzi unaoweza kuonekana kwa macho ya nyama, ni ulinzi maalumu unaotokana na uhusiano bora kati ya Ayubu na Mungu, inawezekana Ayubu hakuwa anaujua, wala hakuna mtu aliyeweza kuuona kwa macho lakini Shetani katika ulimwengu wa roho alifahamu kuwa Ayubu anazingirwa na ukigo pande zote, ulinzi huu wa Mungu hautokani na juhudi zetu wala haki yetu kwa hiyo sio sisi tunaoweza kuuweka ulinzi huo bali Bwana mwenyewe anawalinda watu wake, hii ni zawadi ya kila aaminiye.

1Petro 1:3-5 “Ahimidiwe Mungu, Baba wa Bwana wetu Yesu Kristo, ambaye kwa rehema zake nyingi alituzaa mara ya pili ili tupate tumaini lenye uzima kwa kufufuka kwake Yesu Kristo katika wafu; tupate na urithi usioharibika, usio na uchafu, usionyauka, uliotunzwa mbinguni kwa ajili yenu. Nanyi mnalindwa na nguvu za Mungu kwa njia ya imani hata mpate wokovu ulio tayari kufunuliwa wakati wa mwisho.”

Sasa ulinzi huo maalumu wa Mungu au nguvu za Mungu zinatotulinda kwa mujibu wa Shetani ameziita ukigo, UKIGO hasa ni nini? Neno ukigo linalotumika katika maandiko hapo katika Lugha ya Kiebrania linasomeka neno “sûk” au neno ώuk” ambalo linatamkwa sook kwa Kiingereza “Hedge” ambalo maana yake ni Ukuta au Ukingo maalumu unaomzingira mtu kwa kusudi la kuweka mipaka ili asizuriwe, it’s a way of protecting oneself against quality loss of financial, circumstances, health garden, properties, flocks etc. ni njia ya kulinda ubora wa mtu, uchumi, mazingira, afya, bustani, mali, na mifugo ili isipatwe madhara  hii ni maana ya kawaida ya UKIGO lakini Ukigo aliouona Shetani katika maisha ya Ayubu ulikuwa ni ukigo wa kiroho, yaani ukigo usioonekana “An unseen hedge” huu sasa ukigo usiionekana ni ukigo wa kiroho unaowekwa na Mungu kwa mtu aliyeokoka kumuwezesha mtu huyo kuwa na ulinzi wa Mungu kwa habari ya maisha yake na mali zake, uchumi wake, afya yake, watoto wake, mifugo yake mashamba yake na kadhalika, An unseen hedge is a spiritual barrier of divine protection placed by God around belivers and their possessions. Kwa hiyo mtu anayemcha Mungu analindwa na Mungu katika ulimwengu wa roho kiasi ambacho shetani analalamika kuwa hawezi kusababisha uharibifu katika jambo lolote kwa sababu Mungu anakulinda.

Kuzingirwa kwa ukigo usioonekana.

Kwa hiyo sasa tunapata ufahamu ya kuwa kila mtu aliyeokoka, kila amwaminiye Mungu, kila aliyeamini, analindwa na Mungu katika ulimwengu wa roho bila yeye mwenyewe kutambua na unaweza kulitambua hilo endapo utaruhusiwa kuona kwa macho ya rohoni, Neno la Mungu linatufunulia hivyo kwamba kila mtu aliyeokoka anazingirwa na UKIGO usioonekana, ulinzi huu hauonekani kwa macho lakini ni halisi, ni ulinzi wa kiroho na hauwezi kuonekana kwa macho ya nyama, ni ulinzi unaowekwa na Mungu mwenyewe na sio kwa jitihada za kibinadamu, ulinzi huu unazunguka Maisha yako, uhai wako, afya yako, familia yako, mali zako, watu wako, mazingira yako, Tunaweza kujifunza kutokana na Nabii Elisha nyakati za agano la kale namna na jinsi alivyokuwa na utambuzi ya kuwa uko ulinzi katika ulimwengu usioonekana kwa macho ambao unawazingira watu wa Mungu pande zote ona

2Wafalme 6:15-17 “Hata asubuhi na mapema mtumishi wake yule mtu wa Mungu alipoondoka, na kwenda nje, kumbe! Pana jeshi la watu, na farasi na magari, wameuzingira mji ule. Mtumishi wake akamwambia, Ole wetu! Bwana wangu, tufanyeje? Akamjibu, Usiogope; maana walio pamoja nasi ni wengi kuliko wale walio pamoja nao. Elisha akaomba, akasema, Ee Bwana, nakusihi, mfumbue macho yake, apate kuona. Bwana akamfumbua macho yule mtumishi; naye akaona; na tazama, kile kilima kilikuwa kimejaa farasi na magari ya moto yaliyomzunguka Elisha pande zote.”

Unaona hapo tunaona kuwa Elisha alikuwa na ufahamu kuwa analindwa na jeshi kubwa sana la malaika wasioonekana kwa macho ya nyama lakini alipomuombea mtumishi wake naye alipewa uwezo wa kuona na kugundua kuwa kulikuwa na magari ya farasi ya moto yaliyowazunguka pande zote, huu ulikuwa ukigo wa kiroho unaowazingira watumishi wa Mungu pande zote, mtu mmoja alisema ikiwa Elisha wa agano la kale alilindwa kiasi hiki ni wazi kuwa waamini katika Kristo nyakati hizi za agano jipya wanalindwa zaidi na nguvu za Mungu na ukigo usioonekana  katika ulimwengu wa roho, kuliko Elisha ambaye Yesu alikuwa hajamfia Msalabani, ikieleza namna watu wa Mungu wanavyolindwa Biblia iko wazi kwamba kila aliyemwamini Yesu analindwa iwe anajua au hajui

Marko 16:15-18 “Akawaambia, Enendeni ulimwenguni mwote, mkaihubiri Injili kwa kila kiumbe. Aaminiye na kubatizwa ataokoka; asiyeamini, atahukumiwa. Na ishara hizi zitafuatana na hao waaminio; kwa jina langu watatoa pepo; watasema kwa lugha mpya; watashika nyoka; hata wakinywa kitu cha kufisha, hakitawadhuru kabisa; wataweka mikono yao juu ya wagonjwa, nao watapata afya.”

Awaye yote ambaye anamtegemea Mungu na kumcha yeye na kuendelea kukaa katika uwepo wa Mungu kimsingi anajiweka katika ulinzi wa Mungu, kwa sababu hiyo kimsingi kila mtu anayemtumainia Mungu anajiweka katika kuzingirwa kwa ukigo usioonekana, inaweza kuwa malaika, ama ukuta wa moto au ukuta wa shaba na kadhalika na ni Mungu ndiye anayetulinda kupiria serikali yake ya mbinguni, ile mamlaka ya kiungu inahusika na ulinzi wetu

Zaburi 91:1-11 “Aketiye mahali pa siri pake Aliye juu Atakaa katika uvuli wake Mwenyezi. Nitasema, Bwana ndiye kimbilio langu na ngome yangu, Mungu wangu nitakayemtumaini. Maana Yeye atakuokoa na mtego wa mwindaji, Na katika tauni iharibuyo. Kwa manyoya yake atakufunika, Chini ya mbawa zake utapata kimbilio; Uaminifu wake ni ngao na kigao. Hutaogopa hofu ya usiku, Wala mshale urukao mchana, Wala tauni ipitayo gizani, Wala uele uharibuo adhuhuri, Ijapo watu elfu waanguka ubavuni pako. Naam, kumi elfu mkono wako wa kuume! Hata hivyo hautakukaribia wewe. Ila kwa macho yako utatazama, Na kuyaona malipo ya wasio haki. Kwa kuwa Wewe Bwana ndiwe kimbilio langu; Umemfanya Aliye juu kuwa makao yako. Mabaya hayatakupata wewe, Wala tauni haitaikaribia hema yako. Kwa kuwa atakuagizia malaika zake Wakulinde katika njia zako zote.”

Daniel 6:18-22 “Kisha mfalme akaenda nyumbani kwake, akakesha usiku kucha, akafunga; na vinanda havikuletwa mbele yake; na usingizi wake ukampaa. Asubuhi mfalme akaondoka mapema, akaenda kwa haraka mpaka penye lile tundu la simba. Naye alipolikaribia lile tundu, akamlilia Danieli kwa sauti ya huzuni; mfalme akanena; akamwambia Danieli, Ee Danieli, mtumishi wa Mungu aliye hai, je! Mungu wako, unayemtumikia daima, aweza kukuponya na simba hawa? Ndipo Danieli akamwambia mfalme, Ee mfalme, uishi milele. Mungu wangu amemtuma malaika wake, naye ameyafumba makanwa ya simba, nao hawakunidhuru; kwa kuwa mbele zake mimi nalionekana kuwa sina hatia; tena, mbele yako, Ee mfalme, sikukosa neno.”

Kwa msingi huo kupitia maandiko haya na ufunuo wa neno la Mungu tunajifunza hapa kuwa mtu anayemtegemea na kumtumainia Mungu anazingirwa kwa ukigo usioonekana katika ulimwengu wa roho ni pale tu unapokuwa na macho ya rohoni na unapolielewa neno la Mungu ndipo unapoweza kuelewa ya kuwa katika ulimwengu wa roho tunao ukigo usioonekana yaani tunao ulinzi usioonekana kwa macho.                             

Jinsi ya kuzingirwa na ukigo usioonekana.

Tunahakikishiwa kuwa ukigo usioonekana ni Dhahiri kwa watu wa Mungu, na ni wa muhimu, lakini swali kubwa ni kuwa tunawezaje kuzingirwa na ukigo huu usiioonekana je tunaweza kuomba ulinzi wa Mungu? Maandiko yanaonyesha wazi kuwa sio dhambi kuomba ulinzi wa Mungu, japokuwa Mungu mwenyewe huwa anawalinda watu wake kwa hiyari yake na mapenzi yake, Shetani alipolaumu kuhusu ulinzi wa Ayubu alisema wewe umemzingira kwa ukigo pande zote maana yake ilikuwa ni Mungu kwa hiyari yake na kwa mapenzi yake alimlinda Ayubu

Ayubu 1:7-10 “Bwana akamwuliza Shetani, Umetoka wapi wewe? Ndipo Shetani akamjibu Bwana, na kusema, Natoka katika kuzunguka-zunguka duniani, na katika kutembea huku na huku humo. Kisha Bwana akamwuliza Shetani, Je! Umemwangalia huyo mtumishi wangu Ayubu? Kwa kuwa hapana mmoja aliye kama yeye duniani, mtu mkamilifu na mwelekevu, mwenye kumcha Mungu na kuepukana na uovu. Ndipo Shetani akamjibu Bwana, na kusema, Je! Huyo Ayubu yuamcha Bwana bure? Wewe hukumzingira kwa ukigo pande zote, pamoja na nyumba yake, na vitu vyote alivyo navyo? Kazi za mikono yake umezibarikia, nayo mali yake imeongezeka katika nchi.”

Hata hivyo ingawa ulinzi wa Mungu ni tukio la hiyari linalofanywa na Mungu mwenyewe maandiko hayakatazi kuomba ulinzi wa Mungu, viko viashiria kadhaa wa kadha vya kimaandiko vinavyotuthibitishia kuwa tunaweza kuomba ulinzi wa Mungu na huu ni ukweli usioweza kupingika, mfano katika sala ya Bwana iliyofundishwa na Bwana Yesu kuna sehemu ya kujiombea ulinzi, lakini sio hivyo tu Yesu katika maombi yake yeye mwenyewe alituombea ulinzi

Mathayo 6:13 “Na usitutie majaribuni, lakini utuokoe na yule mwovu. [Kwa kuwa ufalme ni wako, na nguvu, na utukufu, hata milele. Amina.]”   

Yohana 17:14-16 “Mimi nimewapa neno lako; na ulimwengu umewachukia; kwa kuwa wao si wa ulimwengu, kama mimi nisivyo wa ulimwengu. Mimi siombi kwamba uwatoe katika ulimwengu; bali uwalinde na yule mwovu. Wao si wa ulimwengu, kama mimi nisivyo wa ulimwengu.”

Ezra 8:21-23 “Ndipo nikaamuru kufunga, hapo penye mto Ahava, ili tupate kujinyenyekeza mbele za Mungu, na kutafuta kwake njia iliyonyoka, kwa ajili yetu sisi wenyewe, na kwa ajili ya watoto wetu, na kwa mali yetu yote. Maana naliona haya kumwomba mfalme kikosi cha askari na wapanda farasi, ili kutusaidia juu ya adui njiani; kwa maana tulikuwa tumesema na mfalme, tukinena, Mkono wa Mungu u juu ya watu wote wamtafutao, kuwatendea mema; bali uweza wake na ghadhabu yake ni kinyume cha wote wamwachao. Basi tukafunga, tukamsihi Mungu wetu kwa ajili ya hayo; naye akatutakabali.”

Kwa hiyo tunajifunza ya kwamba mojawapo ya njia ya kuzingirwa na ukigo usioonekana ni pamoja na kuomba ulinzi wa Mungu kwaajili yetu japo kuwa swala la kulindwa na Mungu liko katika mikono yake, na sisi tu mali yake  

Njia nyingine ya kukaribisha ulinzi wa Mungu au kuzingirwa na ukigo usioonekana katika maisha yetu ni kuwa na Maisha ya kumcha Mungu, Neno la Mungu linathuthibitishia ya kuwa Mungu huwazingira kwa ngao wale wanaotembea katika haki yaani wale wanaomcha Mungu.

Zaburi 5:11-12 “Nao wote wanaokukimbilia watafurahi; Watapiga daima kelele za furaha. Kwa kuwa Wewe unawahifadhi, Walipendao jina lako watakufurahia. Kwa maana Wewe utambariki mwenye haki; Bwana, utamzungushia radhi kama ngao.”

Zaburi 34:7-9 “Malaika wa Bwana hufanya kituo, Akiwazungukia wamchao na kuwaokoa. Onjeni mwone ya kuwa Bwana yu mwema; Heri mtu yule anayemtumaini. Mcheni Bwana, enyi watakatifu wake, Yaani, wamchao hawahitaji kitu.”

Ulinzi wa Mungu unathibitika wazi kwa wale wanaomcha Mungu, ni muhimu kufahamu kuwa ahadi za Mungu zinategemea (Conditional) pande zote mbili, Mungu anatoa ahadi ya kutupigania na kutulinda lakini ni wajibu wetu kumtii, kama utaharibu ukigo wako wewe mwenyewe utauharibu kwa kutokuwa mwaminifu kwa Mungu na hapo ni lazima utakula mkong’oto, hapa nisikupake mafuta kwa mgongo wa chupa niweke wazi kuwa kama ukimkosea Mungu huna budi kutubu na kurekebisha kwa haraka usitegemee ulinzi wa Mungu wakati wa kuasi kinyume na mapenzi yake ndio maana siku hizi hata walokole wanarogwa! Wanarogwaje kwa sababu wanaishi maisha ya kawaida na kuendelea katika dhambi huku wakidhani Mungu anatendelea kuwa mlinzi kwao tuambiane ukweli usimpe ibilisi nafasi, Mungu alimuhakikishia Joshua ushindi yaani maana yake pamoja na ulinzi lakini sharti ilikuwa lazima atende sawasawa  na yote yaliyoandika katika kitabu cha torati ya Musa vinginevyo unapigwa ona:-

Yoshua 1:5-7 “Hapatakuwa mtu ye yote atakayeweza kusimama mbele yako siku zote za maisha yako; kama nilivyokuwa pamoja na Musa, ndivyo nitakavyokuwa pamoja na wewe; sitakupungukia wala sitakuacha.Uwe hodari na moyo wa ushujaa, maana ni wewe utakayewarithisha watu hawa nchi hii niliyowaapia baba zao ya kwamba nitawapa. Uwe hodari tu na ushujaa mwingi, uangalie kutenda sawasawa na sheria yote aliyokuamuru Musa mtumishi wangu; usiiache, kwenda mkono wa kuume, au wa kushoto, upate kufanikiwa sana kila uendako.”

Yoshua 7:1-12 “Lakini wana wa Israeli walifanya dhambi katika kitu kilichowekwa wakfu; maana Akani, mwana wa Karmi, mwana wa Zabdi, mwana wa Zera, wa kabila ya Yuda, alitwaa baadhi ya vitu vilivyowekwa wakfu; hasira ya Bwana ikawaka juu ya wana wa Israeli. Kisha Yoshua akatuma watu kutoka Yeriko mpaka mji wa Ai, ulio karibu na Bethaveni, upande wa mashariki wa Betheli, akawaambia, akisema, Pandeni juu mkaipeleleze nchi, basi wakapanda juu wakaupeleleza Ai. Wakarejea kwa Yoshua wakamwambia, Wasiende watu wote, ila waende watu kama elfu mbili, tatu, wakaupige Ai; usiwataabishe watu wote kwa kuwaendesha huko; maana watu hao ni wachache tu. Basi watu wakaenda huko wapata elfu tatu tu; nao wakakimbia mbele ya watu wa Ai. Watu wa Ai wakawapiga watu kama thelathini na sita; wakawafuatia kutoka mbele ya mlango mpaka Shebarimu, wakawapiga huko kwenye matelemko; mioyo ya watu ikayeyuka, ikawa kama maji. Yoshua akararua mavazi yake, akaanguka kifudifudi mbele ya sanduku la Bwana hata jioni, yeye na wazee wa Israeli; wakatia mavumbi vichwani mwao. Yoshua akasema, Ee Bwana MUNGU, kwa nini umewavusha watu hawa mto wa Yordani, ili kututia katika mikono ya Waamori, na kutuangamiza? Laiti tungelikuwa radhi kukaa ng'ambo ya Yordani Ee Bwana, niseme nini baada ya Israeli kuwapa visogo adui zao? Maana Wakanaani na wenyeji wote wa nchi hii watasikia habari hii, nao watatuzingira, na kulifuta jina letu katika nchi. Nawe utafanya nini kwa ajili ya jina lako kuu? Bwana akamwambia Yoshua, Haya! Inuka, mbona umeanguka kifudifudi hivi? Israeli wamefanya dhambi, naam, wamelivunja agano langu nililowaagiza; naam, wametwaa baadhi ya vitu vilivyowekwa wakfu; tena wameiba, tena wameficha na kuvitia pamoja na vitu vyao wenyewe. Ndiposa wana wa Israeli hawawezi kusimama mbele ya adui zao; wakawapa visogo adui zao, kwa sababu wamelaaniwa; mimi sitakuwa pamoja nanyi tena, msipokiharibu kitu kile mlicho nacho kilichowekwa wakfu.”

Kumbukumbu 1:41-45 “Ndipo mkanijibu, mkaniambia, Sisi tumefanya dhambi juu ya Bwana, tutakwea kupigana kwa mfano wa yote tuliyoamriwa na Bwana. Mkajifunga kila mtu silaha zake za vita, mkafanya wepesi kukwea mlimani. Bwana akaniambia, Uwaambie, Msiende, wala msipigane; kwani mimi si kati yenu; msije mkapigwa mbele ya adui zenu. Basi niliwaambia, msinisikize, bali mliasi amri ya Bwana, mkajikinai, na kukwea mlimani. Na Waamori waliokuwa wakikaa katika mlima huo, waliwatokea juu yenu, wakawafukuza, kama wafukuzwao na nyuki, wakawapomoshea Seiri mpaka Horma. Mkarudi mkalia mbele za Bwana; Bwana asiisikize sauti yenu, wala hakuelekeza masikio yake kwenu.”             

Neno la Mungu linatufundisha wazi hapo kuwa ulinzi wa Mungu ni Dhahiri kwa wale wamchao, lakini kama tukimuasi tunakuwa tumeharibu ukigo unaotuzingira na kwa sababu hiyo ni rahisi kushindwa na kushambuliwa na inaweza kuwa aibu kwetu, kama watu wanamtaka Mungu basi wamtake jumla jumla na sio nusu nusu, Neno la Mungu linasema yeye abomoaye boma nyoka watamuuma

Muhubiri 10:8-9 “Mwenye kuchimba shimo atatumbukia ndani yake; Na yeye abomoaye boma, nyoka atamwuma. Mwenye kuchonga mawe ataumizwa kwayo; Naye apasuaye miti huona hatari katika hiyo.”    

Kama hujaokoka na unahitaji ulinzi wa Mungu basi ni vema ukampokea Yesu,awe bwana na mwokozi wa maisha yako, Damu ya Yesu ni ulinzi na usalama wa maisha yako na Yule muharibifu anapoona alama ya damu yeye atapita juu yako na hataleta madhara katika nyumba yako kwa sababu umeiamini ile kazi iliyofanywa naye pale Msalabani.

Kutoka 12:12-13 “Maana nitapita kati ya nchi ya Misri usiku huo, nami nitawapiga wazaliwa wa kwanza wote katika nchi ya Misri, wa mwanadamu na wa mnyama; nami nitafanya hukumu juu ya miungu yote ya Misri; Mimi ndimi BWANA. Na ile damu itakuwa ishara kwenu katika zile nyumba mtakazokuwamo; nami nitakapoiona ile damu, nitapita juu yenu, lisiwapate pigo lo lote likawaharibu, nitakapoipiga nchi ya Misri.”

Kuzingirwa na ukigo usioonekana ni swala la uhakika kwa wana wa Mungu, Nanyi mnalindwa na nguvu za Mungu, ukweli tunaweza tusione kwa macho kile kinachoendelea katika ulimwengu wa roho lakini neno la Mungu linatuhibitishia kuwa tunalindwa, malaika wapo, ukuta wa moto uko unatuzunguka na mbingu zinatambua uwepo wetu na mahitaji yetu na wema wake utatuzunguka

Zakarika 2:5 “Kwa maana mimi, asema Bwana, nitakuwa ukuta wa moto kuuzunguka pande zote, nami nitakuwa huo utukufu ndani yake.”

Na. Rev. Innocent Samuel Kamote

Mkuu wa wajenzi mwenye Hekima        

Alhamisi, 1 Januari 2026

Nyakati za kuburudishwa!


Matendo 3:18-20 “Lakini mambo yale aliyohubiri Mungu tangu zamani kwa kinywa cha manabii wake wote, ya kwamba Kristo wake atateswa, ameyatimiza hivyo. Tubuni basi, mrejee, ili dhambi zenu zifutwe, zipate kuja nyakati za kuburudishwa kwa kuwako kwake Bwana; apate kumtuma Kristo Yesu mliyewekewa tangu zamani;”




Utangulizi:

Kwa kawaida mojawapo la hitaji kubwa la kila mwanadamu duniani ni pamoja na kupata wakati wa kupumzika au kuburudishwa, Mwanadamu anapopata pumziko na kuburudishwa anapata nafasi ya kuwa na utulivu na kujijenga upya kimwili, kiakili, kihisia, kiroho na kisaikolojia, hivyo kumwezesha kupata nafasi ya kujijenga na kujitia nguvu kwa upya, Mwanadamu sio mashine au robot kwa sababu hiyo anaweza kuchoshwa na mambo mengi na hivyo anahitaji kupumzika, wakati huo wa mapumziko mwanadamu anahitaji kuburudishwa ili aweze kuwa vizuri kwaajili ya majukumu mengine mazuri zaidi, Mungu anafahamu sana kuwa wanadamu wanahitaji mapumziko ili waweze kujijenga upya.

Mathayo 11:28-29 “Njoni kwangu, ninyi nyote msumbukao na wenye kulemewa na mizigo, nami nitawapumzisha. Jitieni nira yangu, mjifunze kwangu; kwa kuwa mimi ni mpole na mnyenyekevu wa moyo; nanyi mtapata raha nafsini mwenu;”

Mapumziko ya mwanadamu yanaweza kumsaidia mwanadamu kuwa na nguvu katika maeneo yote ya maisha, kuwa na uwezo wa kustahimili migandamizo ya mawazo, kujenga mawazo mapya, kuwa na uwezo wa kutafakari, kupunguza mawazo, kuabudu, kupumzisha akili, kupokea mtazamo mpya, kuwa na mitazamo chanya, kusahau maumivu, na kuleta ufanisi unaomuondoa mwanadamu katika kuishi maisha ya mambo yanayojirudia rudia tena na tena kwa hiyo kuburudika ni hitaji kubwa la kiroho la Mwanadamu na ndio maana wanadamu wana likizo, mapumziko na usingizi n.k. ili kujikarabati, hata hivyo leo tutaangalia kwa undani na kwa kina namna ambayo Mungu huleta nyakati za kuburudishwa kwa wanadamu hasa pale wanapotubu na kurejea na kupokea msamaha wa Mungu kwa imani katika Kristo Yesu. Tutajifunza somo hili Nyakati za kuburudishwa kwa kuzingatia maswala muhimu yafuatayo:-

·         Maana ya nyakati za kuburudishwa.

·         Mwanadamu na nyakati za kuburudishwa.

·         Jinsi ya kuwa na nyakati za kuburudishwa.

Maana ya nyakati za kuburudishwa.

Matendo 3:18-20 “Lakini mambo yale aliyohubiri Mungu tangu zamani kwa kinywa cha manabii wake wote, ya kwamba Kristo wake atateswa, ameyatimiza hivyo. Tubuni basi, mrejee, ili dhambi zenu zifutwe, zipate kuja nyakati za kuburudishwa kwa kuwako kwake Bwana; apate kumtuma Kristo Yesu mliyewekewa tangu zamani;”

Tunaona katika kifungu hiki neno la Mungu likizungumzia na kuwaita watu watubu na kurejesha uhusiano wao na Mungu ili kwamba wapate nyakati za kuburudishwa kwa uwepo wa Bwana, ni muhimu kwetu sasa kujiuliza kwamba neno kuburudishwa hasa lina maana gani?, Neno kuburudishwa kimsingi linalotajwa hapo katika neno la asili la Kiyunani linasomeka kama “Anapsuxis” au “Anapaύō” kwa kiingereza “refreshing” – Properly a recovery of breath ambalo maana yake ni kupumzika, kuhuishwa, kutulia ili kupata nguvu kwa upya, kujipa unafuu, kujituliza, kupunga upepo, kutuliza akili, kutuliza roho mwili na nafsi,  au kuvuta pumzi, kuburudika, kujipa nafasi, raha, kupata pumzi mpya, kurejeshea nguvu zilizopotea, kurudishia pumzi kwa usawia!.

Kutoka 23:12 “Siku sita utafanya kazi yako, na siku ya saba utapumzika; ili kwamba ng'ombe wako na punda wako wapate kupumzika, kisha mwana wa mjakazi wako na mgeni wapate kuburudika.”

2Samuel 16:13-14 “Basi wakaendelea njiani Daudi na watu wake; Shimei naye akaaendelea juu ya ubavu wa kile kilima, kwa kumkabili, huku akiendelea, akilaani, akimtupia mawe, na kurusha mavumbi. Naye mfalme na watu wake wote waliokuwa pamoja naye wakafika, wamechoka sana; naye akajiburudisha huko.”

1Wakorintho 16:17-18 “Nami nafurahi kwa sababu ya kuja kwao Stefana na Fortunato na Akaiko; maana hawa wamenikirimia kwa wingi yale niliyopungukiwa kwenu. Maana wameniburudisha roho yangu, na roho zenu pia; basi wajueni sana watu kama hao.”

Warumi 15:30-32 “Ndugu zangu, nawasihi kwa Bwana wetu Yesu Kristo, na kwa upendo wa Roho, jitahidini pamoja nami katika maombi yenu kwa ajili yangu mbele za Mungu; kwamba niokolewe na wale wasioamini katika Uyahudi, na tena huduma yangu niliyo nayo huko Yerusalemu ikubalike kwa watakatifu;nipate kufika kwenu kwa furaha, kama apendavyo Mungu, nikapate kupumzika pamoja nanyi.”

Kwa hiyo kimsingi kupumzika kwa mwanadamu kuna uhusiano mkubwa sana na uwepo wa Mungu Roho Mtakatifu, Mwanadamu anaweza kujipa raha au pumziko la kimwili tu lakini pumziko hilo sio pumziko la uhakika likilinganishwa na pumziko analolitoa Bwana wetu Yesu Kristo endapo mtu atampokea, tunafunuliwa katika andiko hilo kwamba, mwanadamu awapo dhambini yuko katika wakati wa kutumikishwa, yuko matesoni, anafanyishwa kazi bila hiyari yake, anatumikishwa na Shetani bila kupenda anateseka na kuelemewa na mizigo  na mateso ya aina mbalimbali na kuwa Pumziko la kweli linapatikana kwa kukubali mwaliko wake Yesu Kristo pekee, aidha mwanadamu anapokuwa katika magonjwa pia yuko vitani mwili wake unapigana kupambana na magonjwa lakini anapopokea uponyaji wa mwili wake nafsi yake na roho yake anapata nafasi ya kupumzika na Yesu Kristo anauwezo wa kutoa pumziko hilo kuanzia nasfini mwetu anauwezo wa kutupumzisha.

Mathayo 11:28-29 “Njoni kwangu, ninyi nyote msumbukao na wenye kulemewa na mizigo, nami nitawapumzisha. Jitieni nira yangu, mjifunze kwangu; kwa kuwa mimi ni mpole na mnyenyekevu wa moyo; nanyi mtapata raha nafsini mwenu;”

Kwa hiyo tunajifunza hapo kuwa nyakati za kuburudishwa ni wakati ambapo Mungu anampa mwanadamu pumzi mpya ya uhai, na kuuhisha roho yake iliyochoka na kukata tamaa kwa sababu ya mapito ya dunia baada ya kukubali toba na kumuamini Bwana Yesu kama Bwana na mwokozi.

Mwanadamu na nyakati za kuburudishwa.

Kila mwanadamu anahitaji nyakati za kuburudishwa aliyeokoka na hata asiyeokoka wote wanahitaji burudiko la kweli kwa sababu ya uchovu wa safari za duniani, Mwanadamu aliumbwa awe na nyakati za kuburudika na kupumzika kila wakati na kila siku, Mungu alipomuweka mwanadamu katika bustani ya Edeni alimuwekea mwanadamu mazingira ya mapumziko na wakati wa kuwa na ushirika na yeye, anguko la mwanadamu limesababisha upungufu mkubwa katika maisha ya mwanadamu, Mwanadamu ni kiumbe na ni kiumbe cha kibaiolojia, chenye utashi na akili na hisia lakini zenye mipaka, baada ya anguko mwanadamu amewekewa mazingira magumu ya kula kwa jasho, kushambuliwa na adui zake, uadui wetu mapepo na na shetani, michongoma na miiba kutuzalia na kuzaa kwa uchungu adhabu zote zile zilizotamkwa na Mungu zimemwekea mwanadamu mazingira ya kuchoka kiroho, kimwili, kiakili, kisaokolojia na kibailojia, hivi vyote vinamfanya mwanadamu kuwa mchovu katika safari ya maisha na kumfanya mwanadamu awe mwenye kuhitaji mapumziko.

Mwanzo 3:9-19 “BWANA Mungu akamwita Adamu, akamwambia, Uko wapi? Akasema, Nalisikia sauti yako bustanini, nikaogopa kwa kuwa mimi ni uchi; nikajificha. Akasema, Ni nani aliyekuambia ya kuwa u uchi? Je! Umekula wewe matunda ya mti niliyokuagiza usiyale? Adamu akasema, Huyo mwanamke uliyenipa awe pamoja nami ndiye aliyenipa matunda ya mti huo, nikala. BWANA Mungu akamwambia mwanamke, Nini hili ulilolifanya? Mwanamke akasema, Nyoka alinidanganya, nikala. BWANA Mungu akamwambia nyoka, Kwa sababu umeyafanya hayo, umelaaniwa wewe kuliko wanyama wote, na kuliko hayawani wote walioko mwituni; kwa tumbo utakwenda, na mavumbi utakula siku zote za maisha yako; nami nitaweka uadui kati yako na huyo mwanamke, na kati ya uzao wako na uzao wake; huo utakuponda kichwa, na wewe utamponda kisigino. Akamwambia mwanamke, Hakika nitakuzidishia uchungu wako, na kuzaa kwako; kwa utungu utazaa watoto; na tamaa yako itakuwa kwa mumeo, naye atakutawala. Akamwambia Adamu, Kwa kuwa umeisikiliza sauti ya mke wako, ukala matunda ya mti ambao nalikuagiza, nikisema, Usiyale; ardhi imelaaniwa kwa ajili yako; kwa uchungu utakula mazao yake siku zote za maisha yako; michongoma na miiba itakuzalia, nawe utakula mboga za kondeni; kwa jasho la uso wako utakula chakula, hata utakapoirudia ardhi, ambayo katika hiyo ulitwaliwa; kwa maana u mavumbi wewe, nawe mavumbini utarudi.

Tangu baada ya anguko la mwanadamu, hitaji la kupumzika limekuwa ni sehemu ya uhitaji mkubwa wa mwanadamu, sio kimwili tu na hata kiroho na nafsi, hitaji la kupumzika na kuburudika linaonyesha kuwa mwanadamu sio kiumbe mkamilifu na wala hajitoshelezi bila Mungu, na kama mtu anaweza kushindana na hitaji la kuburudika na kupumzika ni wazi kuwa anashindana na asili, kwani hata zaidi ya maisha ya asili mwanadamu anahitaji kuburudika kiroho na hapo ndipo anapopata Amani, kugundua kusudi la kuwepo kwake na kujikuta anakamilika kwa hiyo katika ulimwengu wa anguko tunahitaji pumziko, Dhambi imeleta uhitaji mkubwa wa mapumziko, wanadamu walianza kutafuta faraja kila wakati katika safari ya maisha mara baada ya anguko ona

Mwanzo 4:20-22 “Ada akamzaa Yabali; huyo ndiye baba yao wakaao katika hema na kufuga wanyama. Na jina la nduguye aliitwa Yubali; huyo ndiye baba yao wapigao kinubi na filimbi. Sila naye akamzaa Tubal-kaini, mfua kila chombo cha kukatia, cha shaba na cha chuma; na umbu lake Tubal-kaini alikuwa Naama.”

Wanadamu walioanguka walijaribu kufanya mambo mbalimbali ya kuwaletea burudani ikiwa ni pamoja na kugundua na kutengeneza vyombo vya muziki kama kinubi na filimbi ili kujaribu kujituliza lakini hata hivyo faraja hizo zote walizojibunia wanadamu hazikuweza kuwaletea amani             ya kweli.

-          Utumwa wa dhambi unachosha - Dhambi ilikuwa imemtenganisha mwanadamu na Mungu, maovu yetu yaliuficha uso wake roho ya mwanadamu ikakumbwa na ukavu na kukosekana kwa utoshelevu bila utoshelevu wa kiungu kwa kweli mwanadamu anakabiliwa na uchovu na ukavu na hitaji la burudiko la mwili nafsi na roho

 

Isaya 59:1-2 “Tazama, mkono wa Bwana haukupunguka, hata usiweze kuokoa wala sikio lake si zito, hata lisiweze kusikia; lakini maovu yenu yamewafarikisha ninyi na Mungu wenu, na dhambi zenu zimeuficha uso wake msiuone, hata hataki kusikia.”

 

Zaburi 32:3-4 “Niliponyamaza mifupa yangu ilichakaa Kwa kuugua kwangu mchana kutwa. Kwa maana mchana na usiku Mkono wako ulinilemea. Jasho langu likakauka hata nikawa Kama nchi kavu wakati wa kaskazi.”       

 

Moyo wa mwanadamu ni kama ardhi kavu wakati wa joto au kiangazi, uwepo wa Mungu ni kama maji, wakati roho zetu zinapokaukiwa tunahitaji nyakati za kuburudishwa na burudiko hili na kiu hii inaweza kutimizwa na Mungu peke yake na haiwezi kupozwa na mwanadamu wala katika mazingira ya kibinadamu.

 

-          Kila mwanadamu anachoka – Ukiwa mwanadamu katika safari hii ya maisha kuna kuchoka, watu wanachoka kimwili kiroho na Kisaikolojia, nafsini mwao na wanaumia kwa hiyo kila mwanadamu anahitaji kutiwa nguvu kwa upya na anayeweza kuwapa nguvu wanaochoka na kuzimia ni Bwana mwenyewe kupitia uwepo wake.  

 

Isaya 40:29-31 “Huwapa nguvu wazimiao, humwongezea nguvu yeye asiyekuwa na uwezo. Hata vijana watazimia na kuchoka, na wanaume vijana wataanguka;bali wao wamngojeao Bwana watapata nguvu mpya; watapanda juu kwa mbawa kama tai; watapiga mbio, wala hawatachoka; watakwenda kwa miguu, wala hawatazimia.”

 

-          Mateso yanachosha sana – Kwa kuwa mwanadamu hakuumbiwa shida anapopita katika changamoto na shida za aina mbalimbali hatimaye anachoka, unapokuwa mtumwa wa mazingira, unapokosa uhuru wako mwenyewe, unapotumikishwa na kutumiwa unazidiwa na mateso na kwa sababu hiyo unachoka na kujikuta unahitaji kupumzika

 

Maombolezo 5:1-5 “Ee Bwana, kumbuka yaliyotupata; Utazame na kuiona aibu yetu. Urithi wetu umegeuka kuwa mali ya wageni; Na nyumba zetu kuwa mali ya makafiri. Tumekuwa yatima waliofiwa na baba; Mama zetu wamekuwa kama wajane.Tumekunywa maji yetu kwa fedha; Kuni zetu twauziwa.Watufuatiao wa juu ya shingo zetu; Tumechoka tusipate raha yo yote.”

 

-                Hata kutenda mema kunachosha - Mwanadamu anapotenda mema na wakati mrefu ukapita bila kuona matokeo pia anaweza kuchoka, unaomba, unatoa, unamlilia Mungu, unafunga unakesha lakini huoni matokeo wakati mwingine pia unaweza kuzimia moyo, unatendea mema watu wanakulipa maovu, unafadhili watu wanakuchukulia poa au kukutumia kwa faida hii nayo inachosha kutokana na hali hii watu pia huweza kuchoka kutenda mema.

 

Wagalatia 6:9-10 “Tena tusichoke katika kutenda mema; maana tutavuna kwa wakati wake, tusipozimia roho. Kwa hiyo kadiri tupatavyo nafasi na tuwatendee watu wote mema; na hasa jamaa ya waaminio.”

Kutokana na changamoto za aina mbalimbali anazokuwa amezipitia mwanadamu kila wakati changamoto hizo zinakuchosha na hivyo unajikuta kuwa unahitaji wakati wa kuburudishwa, ukiishi maisha ya utauwa utaudhiwa, ukiishi maisha ya anasa na dhambi utatumikishwa na shetani kwa ujumla duniani tunayo dhiki hata hivyo habari njema ni kuwa ziko nyakati za kuburudishwa hizi ni nyakati zinapatikana kwa toba na kufutiwa dhambi na kupewa wakati wa kuburudishwa, yaani ubatizo wa Roho Mtakatifu, Petro ndiye anatufunulia swala hili katika hutuba yake sikuya Pentekoste anaonyesha kuwa katika Bwana kuna kuburudishwa kila mwanadamu anahitaji nyakati hizi anahitaji burudiko la mwili wake, nasi yake na roho.  Na burudiko hili linapatikana kwa kurejesha uhusiano wetu na Mungu, baada ya toba Roho Mtakatifu anaposhuka ndani ya mwamini anamwezesha kuishi maisha yenye burudiko

Matendo 3:18-20 “Lakini mambo yale aliyohubiri Mungu tangu zamani kwa kinywa cha manabii wake wote, ya kwamba Kristo wake atateswa, ameyatimiza hivyo. Tubuni basi, mrejee, ili dhambi zenu zifutwe, zipate kuja nyakati za kuburudishwa kwa kuwako kwake Bwana; apate kumtuma Kristo Yesu mliyewekewa tangu zamani;”

Jinsi ya kuwa na nyakati za kuburudishwa.

Mungu katika hekima yake anafahamu kuwa wanadamu wanahitaji nyakati za kuburudhishwa na kwa sababu hiyo neno lake limejaa ahadi za kuburudishwa.

Yeremia 31:23-25 “Bwana wa majeshi, Mungu wa Israeli, asema hivi, Watatumia tena neno hili katika nchi ya Yuda, na katika miji yake, nitakapowarudisha mateka yao; Bwana na akubariki, Ee kao la haki, Ee mlima wa utakatifu. Na Yuda, na miji yake yote, watakaa humo pamoja; wakulima, nao waendao huko na huko pamoja na makundi yao. Kwa maana nimeishibisha roho yenye uchovu, nami nimeiridhisha kila roho yenye huzuni.”

Zaburi 68:8-10 “Nchi ilitetemeka Naam, mbingu zilidondoka usoni pa Mungu; Hata Sinai usoni pa Mungu; Mungu wa Israeli.Ee Mungu, ulinyesha mvua ya neema; Urithi wako ulipochoka uliutia nguvu. Kabila yako ilifanya kao lake huko; Ee Mungu, kwa wema wako uliwaruzuku walioonewa.”

Petro anaunganisha toba kama njia ya kuleta amani na burudiko la kweli kwa mwanadamu, lakini zaidi sana anazungumzia ile ahadi ya Roho Mtakatifu ndani ya mtu aliyeamini kwa kutubu dhambi zake kwa kumaanisha kuziacha na kuzijutia, ni ukweli ulio wazi kwa kila mtu kuwa ukijazwa Roho Mtakatifu unakuwa na wakati wa kuburudisha, Petro alikuwa anamzungumzia Roho Mtakatifu ndani ya mwamini anakuwa ni kama maji ya kunywa  na kuoga wakati wa joto, aliyeokoka anakuwa ni kama maji ya mito inayotiririka, Hakuna jambo linaleta furaha na amani kama kumpokea Roho Mtakatifu muulize kila mtu ambaye amejazwa Roho Mtakatifu atakuelezea jinsi ilivyo furaha kubwa sana hata unapopita katika magumu yeye anakupa burudiko lisiloweza kuelezeka.

Matendo 4:24-31. “Hata walipofunguliwa, wakaenda kwa watu wao, wakawapasha habari ya mambo yote waliyoambiwa na wakuu wa makuhani na wazee. Nao waliposikia, wakampazia Mungu sauti zao kwa moyo mmoja, wakisema, Mola, wewe ndiwe Mungu, ndiwe uliyefanya mbingu na nchi na bahari na vitu vyote vilivyomo; nawe ulinena kwa Roho Mtakatifu kwa kinywa cha babaetu Daudi, mtumishi wako, Mbona mataifa wamefanya ghasia, Na makabila wametafakari ubatili? Wafalme wa dunia wamejipanga, Na wakuu wamefanya shauri pamoja Juu ya Bwana na juu ya Kristo wake. Maana ni kweli, Herode na Pontio Pilato pamoja na Mataifa na watu wa Israeli, walikusanyika katika mji huu juu ya Mtumishi wako mtakatifu Yesu, uliyemtia mafuta, ili wafanye yote ambayo mkono wako na mashauri yako yamekusudia tangu zamani yatokee. Basi sasa, Bwana, yaangalie matisho yao; ukawajalie watumwa wako kunena neno lako kwa ujasiri wote, ukinyosha mkono wako kuponya; ishara na maajabu vifanyike kwa jina la Mtumishi wako mtakatifu Yesu.Hata walipokwisha kumwomba Mungu, mahali pale walipokusanyika pakatikiswa, wote wakajaa Roho Mtakatifu, wakanena neno la Mungu kwa ujasiri.”

2Wakorintho 4:8-9 “Pande zote twadhikika, bali hatusongwi; twaona shaka, bali hatukati tamaa; twaudhiwa, bali hatuachwi; twatupwa chini, bali hatuangamizwi;”

Uwepo wa Roho Mtakatifu ndani ya mtu aliyemwamini Yesu unayafanya maisha kuwa burudani kila wakati unamfanya mtu aliyemwamini Bwana asitikiswe na lolote, awe na nguvu ya kustahimili kwa sababu hata kama kwa nje anateseka kwa ndani kuna bubujiko la burudiko kubwa ndani yake, Roho Mtakatifu anatoa nguvu ya kustahimili, anatoa msaada wa uungu ndani yetu kushinda kila vikwazo vya kibinadamu na vya asili anatutia nguvu analihuisha neno la Mungu ndani yetu na kulifanya liwe na uhai na kukuwezesha kustahimili anakupa neema ya kuliona pendo la Mungu katika mateso na magumu na anakupa kuwacheka na kuwahurumia wanaodhani wanaweza kukukwaza kwa sababu zozote zile ndani yako maneno haya yanakuwa hai na halisi ndani ya mtu aliyeokoka.

Warumi 8:35-39 “Ni nani atakayetutenga na upendo wa Kristo? Je! Ni dhiki au shida, au adha, au njaa, au uchi, au hatari, au upanga? Kama ilivyoandikwa, ya kwamba, Kwa ajili yako tunauawa mchana kutwa, Tumehesabiwa kuwa kama kondoo wa kuchinjwa. Lakini katika mambo hayo yote tunashinda, na zaidi ya kushinda, kwa yeye aliyetupenda. Kwa maana nimekwisha kujua hakika ya kwamba, wala mauti, wala uzima, wala malaika, wala wenye mamlaka, wala yaliyopo, wala yatakayokuwapo, wala wenye uwezo, wala yaliyo juu, wala yaliyo chini, wala kiumbe kinginecho chote hakitaweza kututenga na upendo wa Mungu ulio katika Kristo Yesu Bwana wetu.”                                

Waebrania 12:26-29 “ambaye sauti yake iliitetemesha nchi wakati ule; lakini sasa ameahidi akisema, Mara moja tena nitatetemesha si nchi tu, bali na mbingu pia. Lakini neno lile, Mara moja tena, ladhihirisha kuhamishwa vile viwezavyo kutetemeshwa, kama vitu vilivyoumbwa, vitu visivyoweza kutetemeshwa vikae. Basi kwa kuwa tunapokea ufalme usioweza kutetemeshwa, na mwe na neema, ambayo kwa hiyo tumtolee Mungu ibada ya kumpendeza, pamoja na unyenyekevu na kicho; maana Mungu wetu ni moto ulao.”

Uwepo wa Mungu ukitembea pamoja nawe ni lazima utapoata raha, raha maana yake refreshment yaani kuburudishwa ni katika uwepo wa Mungu kila mmoja wetu ataweza kubudurika hakuna namna nyingine tunapouanza mwendo wa mwaka huu mpya wa 2026 kila mmoja wetu ajikite katika kuutafuta uwepo wa Mungu, Kufanya kazi kwa bidii kutafuta fedha kwa njia za halali bila kuacha kuutafuta uso wa Bwana kwa bidii ili atupe raha, Bwana Mungu na atembee pamoja nawe katika mwaka huu na akupe nyakati za kuburudishwa katika jina la Yesu Kristo aliye hai, ulivyotembea katika nyakati ngumu na za majaribio imetosha sasa ni wakati wako wa kuburudishwa Mungu yuko tayari kutoa raha, na burudiko kwa wanadamu wote waliookolewa n ahata wasiookolewa kila mmoja wetu anahitaji kuburudishwa nami kama Petro alivyotangaza zikujie nyakati za kuburudishwa nakutangazia kuwa tayari kwa kuburudishwa, Pokea uwepo wa Bwana maishani mwako uwe na wakati wa kuburudishwa, mtii Mungu na itii sauti yake zipate kuja nayakati za kuburudishwa kwako katika jina la Yesu Kristo aliye hai. 

Kutoka 33:14-17 “Akasema, Uso wangu utakwenda pamoja nawe, nami nitakupa raha. Naye akamwambia, Uso wako usipokwenda pamoja nami, usituchukue kutoka hapa.Kwa maana itajulikanaje kuwa nimepata neema mbele zako, mimi na watu wako? Siyo kwa sababu unakwenda pamoja nasi, hata mimi na watu wako tutengwe na watu wote walio juu ya uso wa nchi? BWANA akamwambia Musa, Nitafanya na neno hili ulilolinena, kwa maana umepata neema mbele zangu, nami nakujua jina lako.”             

Na. Rev. Innocent Samuel Kamote

Mkuu wa wajenzi mwenye Hekima.