Zaburi 124:6-8 “Na ahimidiwe Bwana;
Asiyetutoa kuwa mawindo kwa meno yao. Nafsi yetu imeokoka kama ndege Katika
mtego wa wawindaji, Mtego umevunjika, nasi tumeokoka. Msaada wetu u katika jina
la Bwana, Aliyezifanya mbingu na nchi.”
Utangulizi:
Ni muhimu kufahamu kuwa na hekima
na maarifa yatakayokusaidia kujua namna inavyokupasa kuenenda katika ulimwengu
huu wenye hila nyingi, ili uweze kujihami na kuwa salama, Katika maisha haya
yenye maadui wengi!
Wakati mwingine katika maisha
watakuwepo watu wenye hila, ambao kimsingi, watataka kukudhibiti, au kukuwekea
mipaka katika maisha, huduma, biashara, masomo na kazi na hata kutaka kukupotezea
muda kukutawala na kukukandamiza ili uwatumikie au kile kitu ambacho Mungu
amekiweka ndani yako kisiweze kufanya kazi katika mazingira makuu ya uhuru yaliyokusudiwa na Mungu au ili wewe usitoke
kimaisha na ikiwezekana uendelee kuwa mtumwa wa kazi wajibu na fikra za mtawala
mjanja ambaye anaweza kukunyima njia ya kujichagulia, kukunyima uhuru wa
kujitegemea kuwa na maamuzi yako mwenyewe na kujiendeleza kwa sababu ya hofu
yake, wivu wake au mawazo machafu hila na wao ndio wawe na maamuzi juu ya
maisha yako siku zote angalia:-
Kutoka 1:8-11 “Basi akainuka mfalme mpya
kutawala Misri, asiyemjua Yusufu. Akawaambia watu wake, Angalieni, watu wa wana
wa Israeli ni wengi tena wana nguvu kuliko sisi. Haya! Na tuwatendee kwa akili,
wasije wakaongezeka; tena, ikitokea vita, wao nao wasije wakashikamana na adui
zetu na kupigana nasi, na kutoka katika nchi hii. Basi wakaweka wasimamizi juu
yao wawatese kwa mizigo yao. Nao wakamjengea Farao miji ya kuwekea akiba,
Pithomu na Ramesesi”
Hali kama hii ndio ilikuwa sababu
kubwa ya mtawala mpya katika Misri kuwaogopa Israel na kuanza kuweka mitego ya
kuwadhoofisha ili ikiwezekana waweze kumezwa na wamisri na kufutika juu ya uso
wa Dunia, kama sio mkono wa Mungu ulioonyooshwa na kuwatetea isingelikuwa
rahisi Israel kutoka Misri, Hali hii sio stori ya Israel tu ni stori ya kila
mtu amwaminiye Mungu duniani katika mikono ya adui yetu mkuu shetani na
maajenti wake ambaye ndiye anataka kuitawala nafsi yako!.
Daudi na watu wake wanamshukuru
Mungu kwa ukombozi wake na kwa mkono wake ulionyooshwa hata kuwapa Israel ushindi,
inaonekana wazi kabisa ujanja wa adui ulikuwa wa kimkakati na wenye ulaghai
mwingi sana, adui alikuwa amejipanga kuwatumikisha watu wa Mungu na kuwabana kiasi ambacho wasingeliweza kupata
msaada; mwenyewe anaona mpango wa adui ulikuwa ni kuwameza wakiwa hai, Kumezwa
ukiwa hai ni kuchukuliwa mateka na kunyimwa uhuru wako huku ukiteswa nafsi yako
na kutumikishwa ukiwa umefungwa kabisa kiasi ambacho ni mpaka
usaidiwe na mtu wa nje hivi ndivyo adui alivyokuwa amemkusudia Daudi na jamii
yake iliyokuwa ikimzunguka. Ona:-
Zaburi 124:1-5 “Kama si Bwana aliyekuwa
pamoja nasi, Israeli na aseme sasa, Kama si Bwana aliyekuwa pamoja nasi,
Wanadamu walipotushambulia. Papo hapo wangalitumeza hai, Hasira yao ilipowaka
juu yetu Papo hapo maji yangalitugharikisha, Mto ungalipita juu ya roho zetu;
Papo hapo yangalipita juu ya nafsi zetu Maji yafurikayo”
Daudi anaizungumzia hali
iliyoikuta nafsi yake na jamii yake sawa na ndege aliyetegewa mtego kisha
akakamatika na kuwekwa tunduni, ndege huyu angekosa uhuru wake na maamuzi yake
na angetawaliwa maisha yake yangekuwa chini ya amri ya aliyemkamata na kumwekea
mtego tu, kama ndege asiyekuwa na nguvu katika mikono ya utawala wa watega
mitego isingekuwa rahisi kupata ukombozi mpaka mtu mwenye nguvu zaidi aje
akukomboe, Kwa hiyo Daudi na wenzake wanauona wokovu walioupata kuwa sio swala
la kubahatisha bali ni tendo la Mungu
mwenye nguvu kuingilia kati na kuivunja mitego ya adui na ndipo nafsi zao
zikaokoka na ndio maana katika Zaburi hii anamhimidi Bwana ambaye alizuia kwa
namna zote wao kuwa mawindo ya adui na kuwaokoa:-
Wakolosai 1:13-14 “Naye alituokoa katika
nguvu za giza, akatuhamisha na kutuingiza katika ufalme wa Mwana wa pendo lake;
ambaye katika yeye tuna ukombozi, yaani, msamaha wa dhambi;”
Leo katika mpango wa Mungu
tutachukua muda kujifunza somo hili “Nafsi
yangu imeokoka kama ndege” kwa kuzingatia vipengele vitatu muhimu
vifuatavyo:-
·
Ndege katika mtego wa wawindaji.
·
Nafsi katika mitego ya wawindaji.
·
Nafsi yangu imeokoka kama ndege.
Ndege katika mtego wa wawindaji.
Zaburi 124:6-8 “Na ahimidiwe Bwana;
Asiyetutoa kuwa mawindo kwa meno yao. Nafsi yetu imeokoka kama ndege Katika
mtego wa wawindaji, Mtego umevunjika, nasi tumeokoka. Msaada wetu u katika jina la Bwana,
Aliyezifanya mbingu na nchi.”
Ni muhimu kufahamu kuwa kama kuna
viumbe wameumbwa wakiwa na uhuru wa asili, basi Ndege ni kiumbe aliyeumbwa
akiwa na uhuru huo wa asili, wana uhuru wa asili na mpana sana waliopewa na
Mungu, lakini sio hivyo tu ni viumbe ambao Mungu anawajali kiasi kwamba hawana
hofu ya maisha, Mungu mwenyewe anawalisha na kuwatunza kwa kiwango cha ajabu
sana, Ndege wana ulinzi wa ajabu sana kwa mujibu wa Biblia hakuna ndege
anayeanguka bila mbingu kuwa na taarifa, kwa hiyo ndege ni kiumbe chenye ulinzi
wa ajabu kutoka kwa Mungu.
Mwanzo 1:20-22 “Mungu akasema, Maji na
yajawe kwa wingi na kitu kiendacho chenye uhai, na ndege waruke juu ya nchi
katika anga la mbingu. Mungu akaumba nyangumi wakubwa, na kila kiumbe chenye
uhai kiendacho, ambavyo maji yalijawa navyo kwa wingi kwa jinsi zao, na kila
ndege arukaye, kwa jinsi yake; Mungu akaona ya kuwa ni vyema. Mungu
akavibarikia, akisema, Zaeni, mkaongezeke, mkayajaze maji ya baharini, ndege na
wazidi katika nchi.”
Mathayo 6:25-26 “Kwa sababu hiyo
nawaambieni, Msisumbukie maisha yenu, mle nini au mnywe nini; wala miili yenu,
mvae nini. Maisha je! Si zaidi ya chakula, na mwili zaidi ya mavazi? Waangalieni
ndege wa angani, ya kwamba hawapandi, wala hawavuni, wala hawakusanyi ghalani;
na Baba yenu wa mbinguni huwalisha hao. Ninyi je! Si bora kupita hao?”
Mathayo 10:28-31 “Msiwaogope wauuao mwili,
wasiweze kuiua na roho; afadhali mwogopeni yule awezaye kuangamiza mwili na
roho pia katika jehanum. Je! Mashomoro wawili hawauzwi kwa senti moja? Wala
hata mmoja haanguki chini asipojua Baba yenu; lakini ninyi, hata nywele za
vichwa vyenu zimehesabiwa zote. Msiogope basi; bora ninyi kuliko mashomoro
wengi.”
Unaona Mungu amewaumba ndege wawe
na uhuru mpana wa asili, waitamalaki dunia vyovyote wapendavyo, Ndege wanatunzwa
na Mungu, hawaangaiki kulima wala kuweka ghalani, lakini Mungu anawalisha, wana
furaha wana amani, lakini zaidi ya yote Mungu anawajali kiasi ambacho
hawaanguki chini bila mbingu kuwa na taarifa, Lakini changamoto kubwa ya ndege
ni wawindaji, Mwanadamu ni kiumbe wa maana zaidi kuliko ndege, Mungu anamjali
mwanadamu katika namna isiyoweza kuelezeka Mwandishi mmoja mpka akamuhoji
Mungu, Mtu ni kitu gani hata umwangalie
Hata hivyo adui mkubwa wa
mwanadamu ni mwanadamu, Mwanadamu ambaye wakati wewe ukiwa huna madhara kwa mtu
wala huwazii mabaya juu ya mtu, wawindaji wanakuwazia mabaya na wanataka
kuitega nafsi yako, Ndege ni kiumbe dhaifu sana na kuna watu wanataka kumkamata
ili wamweke katika tundu, hapo wanataka ndege awe na uhuru finyu, na walimshe
wao badala ya Mungu, huu ndio mkakati wa shetani, yeye anataka kuikamata nafsi
yako, aifunge akutumikishe usifurahie ule uhuru na maisha uliyopewa na Mungu,
leo hata kama nasfi yako imekamatika ninakutangazia kuwa ni siku ya kwenda
kuzifungulia nasfi zilizofungwa na kuwekewa mipaka katika jina la Yesu Kristo
mwana wa Mungu aliye hai.
Wawindaji sio watu wazuri hata
kidogo, wao mpango wao ni kuikamata nafsi yako, na hili ndilo jangwa kubwa sana
la kiroho hapa duniani yaani pale nafsi
yako inapokuwa imekamatika, Maandiko yanaonyesha kuwa mtu akifanikiwa kuiteka
nafsi yako hususani kama ni adui anaweza kukuweka katika hali ya hatari kubwa
sana na kusababisha uharibifu mkubwa wa kiroho na kuitishia usalama wako na
kukukosesha amani katika maisha, Waandishi wa Zaburi mara kwa mara wameonyesha kuwa
adui anaziwinda nafsi zetu na ili uweze kupata msaada kama umekamatika au
unawindwa basi ni Mungu peke yake ndiye
anayeweza kukusaidia na kukuokoa na kuirejesha nafsi yako katika uhuru wake
ona:-
Zaburi 7:1-2 “Bwana, Mungu wangu,
nimekukimbilia Wewe, Uniokoe na wote wanaonifuatia, uniponye. Asije akaipapura
nafsi yangu kama simba, Akiivunja-vunja pasipokuwa na wa kuponya.”
Zaburi 59:1-3 “Ee Mungu wangu, uniponye na
adui zangu, Uniinue juu yao wanaoshindana nami. Uniponye nao wafanyao maovu,
Uniokoe na watu wa damu. Kwa maana wanaiotea nafsi yangu; Wenye nguvu
wamenikusanyikia; Ee Bwana, si kwa kosa langu, Wala si kwa hatia yangu.”
Mwandishi wa Zaburi hii Daudi
anazungumza kwa lugha ya fumbo au lugha ya kimashairi akilinganisha maisha yake
au nafsi yake kama maisha ya ndege, Ndege ni viumbe dhaifu sana na hawana nguvu
ya kujitetea na wala wengi hawajui kama
wanawindwa au wana maadui, moyo wa ndege wengi ni moyo mwororo na mnyoofu ndege
hawana neno na mtu wao wanapoamka asubuhi hawafikiri kufanya uadui na mtu, wao
huamka na kumtukuza Mungu kisha kuendelea na majukumu yao ya kila siku, hawajui
kama kuna mtu ataamka na kuwawekea mtego, wala hawajui kuwa kuna mtu ataamka na
kuwageuza wao kuwa mfugo au kitoweo au kuwafungua katika tundu hawajui kama
kuna wawindaji, ni muhimu ukaishi maisha yako lakini uwe makini na wawindaji,
wawindaji wako kila mahali!
Lugha hii anayoitumia mwandishi
wa Zaburi inawahusu watu wanaomcha Mungu, wengi wanawindwa nafsi zao lakini
hawajui, wengi huamini kila mtu na wakati mwingine hawajui kama kuna mtu
anaweza kuwa adui na kuziwinda nafsi zao, Ndege anawakilisha udhaifu wa
mwanadamu, Hakuna mwanadamu mwenye nguvu ya kuvunja mitego ya adui Shetani na hata
kujiokoa katika mikono yake, Shetani hutumia njia mbalimbali katika kuhakikisha
kuwa unaingia kwenye mitego yake ikiwa ni pamoja na kuitumia hofu, magonjwa, dhambi,
mauti, na mashambulizi makali kutoka kwa
majeshi yake ya pepo wabaya na watumishi wake wanadamu yaani maajenti wake,
waganga, wachawi, wanga, wenye hila na
wenye wivu,Tunapoishi duniani fahamu na kuelewa kuwa wewe ni dhaifu kama ndege
na bila masaada wa Mungu ni vigumu kwako kuwa huru kama Mungu mwenye nguvu
hatakulinda na kukuepusha na mitego ya wawindaji, kila kitu duniani ulicho
nacho kinawindwa, wewe hujui, ndoa yako inawindwa, kazi yako inawindwa, cheo
chako kinawindwa, mali zako zinawindwa, biashara yako inawindwa, familia yako
inawindwa, masomoni, unawindwa, huduma yako inawindwa, wawindaji ni watu wenye
uchungu, ni wenye wivu, ni wenye nia mbaya, ni wenye hila na wamejaa kila
mahali duniani, hata kwenye genge lako la nyanya pale sokoni, unawindwa, kama
ndege katika mtego wa wawindaji, Bwana akupe neema kuigundua mitego yote
unayotegewa na akuokoe na mitego ya wawaindaji katika jina la Yesu Kristo sema
ameeeen!
Nafsi katika mitego ya wawindaji
Tumeona kuwa maisha ya mwanadamu
ni kama maisha ya ndege katika mitego ya adui, na kinachowindwa katika maisha
yetu mara tu baada ya kuzaliwa kwetu ni Nafsi, Neno nafsi katila lugha ya
kiebrania ni “Nephesh” ambalo
linamaanisha uhai, nafsi au mtu wa ndani, mwanadamu ana sehemu kuu tatu Mwili,
Nafsi na Roho, vita vyetu vyote vya kiroho na kimaamuzi vinafanyika katika
nafsi, nafsi inaponaswa katika mtego ambao unajulikana kama “Pach” Kiebrania ikimaanisha “tanzi”, au mbinu za kunasia, na
wawindaji wanaitwa “Yagosh” Kiebrania
yaani watu wenye hila au wanasao kwa hila, wenye
wivu, wenye uchungu, wasiopenda maendeleo yako, sasa nafsi inapokamatwa
unaingizwa katika utumwa wa mwindaji na huwezi kuachiwa mpaka Mungu aingilie
kati, mtu anapokuendea kwa mganga kukuroga maana yake anaitafuta nafsi yako
aikamate na kuielekeza kule anakotaka yeye, nafsi yako ikikamatwa unaingia
utumwani unamezwa ukiwa hai unapoteza uhuru uliokusudiwa na Mungu katika maisha
yako!, unaona maisha yako ni kama yako gizani nafsi yako imekalishwa mahali
penye giza, watu wamekufunga, umekuwa kama ndege katika tundu unafugwa badala
ya kuwa na uhuru wako mpana wa asili uliokusudiwa na Mungu!
Zaburi 143:3-4 “Maana adui ameifuatia nafsi
yangu, Ameutupa chini uzima wangu. Amenikalisha mahali penye giza, Kama watu
waliokufa zamani. Na roho yangu imezimia ndani yangu, Moyo wangu ndani yangu
umesituka.”
Adui wanapoipata nafsi yako kila
kitu ndani yako na mali yako kinachukuliwa mateka na nafsi yako ndiyo
inayoteseka, na maisha yako yanaharibiwa unatupwa chini, unawekwa kwenye giza
na unakuwepo duniani lakini ni kama mtu aliyekufa, wawindaji wakiishika nafsi
yako wanajivunia majivumo makubwa wanatamba kuwa wamekuweza na huwezi
kufurukuta tena, wamekuweka kwenye kiganja, wokovu wako au ukombozi wako ni
mpaka Bwana pekee aingilie kati, nafsi ikishikwa unakuwa mtumwa huwezi kufanya
unalotaka wala huwezi kufanya mapenzi ya Mungu bali utafanya kile nafsi yako
inakokukokota na adui zako wanakokupeleka, utasikia yule sisi tumemuweka kwenye
kiganja ujue wameishika nafsi yako, Utasikia Bosi mimi haniambii kitu nimemuweka
hapa! ahaa nafsi imeshikwa, Makahaba wanaoiba waume za watu huwa wanatafuta
kuwashika nafsi, wakishawashika, mumeo harudi kwako kwa watai, fedha anapeleka
huko, anapewa raha za ajabu na kupikiwa vizuri ili wewe usahau familia yako na
umtese mkeo wako kwa nini changamoto nafsi ikishatekwa umetekwa maisha yako
yote, ukitaka kumtumikisha mtu mshike nafsi yake, watu wengi wameshikwa na
wanatumika wakati mwingine bila kupenda!
Farao alipowakamata Israel na
kuwaweka kwenye tundu la utumwa nani angeweza kuwafungulia? Ni mpaka mwenye
nguvu alipoingilia kati na kushughulika na adui ndipo Bwana alipowaweka huru!
Ona
Kutoka 15:6-13 “BWANA, mkono wako wa kuume
umepata fahari ya uwezo, BWANA, mkono wako wa kuume wawaseta-seta adui. Kwa wingi
wa ukuu wako wawaangusha chini wanaokuondokea, Wapeleka hasira yako, nayo
huwateketeza kama mabua makavu. Kwa upepo wa mianzi ya pua yako maji
yalipandishwa, Mawimbi yakasimama juu wima mfano wa chungu, Vilindi
vikagandamana ndani ya moyo wa bahari. Adui akasema, Nitafuatia, nitapata,
nitagawanya nyara, Nafsi yangu itashibishwa na wao; Nitaufuta upanga wangu,
mkono wangu utawaangamiza. Ulivuma kwa upepo wako, bahari ikawafunikiza;
Wakazama kama risasi ndani ya maji makuu. Ee BWANA, katika miungu ni nani aliye
kama wewe? Ni nani aliye kama wewe, mtukufu katika utakatifu, Mwenye kuogopwa
katika sifa zako, mfanya maajabu? Ulinyosha mkono wako wa kuume, Nchi
ikawameza. Wewe kwa rehema zako umewaongoza watu uliowakomboa, Kwa uweza wako
uliwaelekeza hata makao yako matakatifu”
Unaona Israel waliposhikwa ni Bwana
ndiye aliyekuja kuwatoa, leo ni siku ambayo kila ambaye ameshikilia nafsi yako
anaiachia kwa mkono wa Bwana ulio hodari ulioonyooshwa katika jina la Yesu!
Nafsi yangu imeokoka kama ndege
Zaburi 124:6-8 “Na ahimidiwe Bwana;
Asiyetutoa kuwa mawindo kwa meno yao. Nafsi yetu imeokoka kama ndege Katika
mtego wa wawindaji, Mtego umevunjika, nasi tumeokoka. Msaada wetu u katika jina la Bwana,
Aliyezifanya mbingu na nchi.”
Mwandishi anaijua historia na
mbinu ya adui kuwa anachikotafuta ni nafsi na anaelewa wazi kuwa nafsi inawindwa
kama ndege na kuwa wenye hila huweka mitego yao ili kutunasa kama ndege na wokovu
wako unaweza kuja kwa namna mbili aidha Mungu akuokoe usiwe mawindo, ASIYETUTOA KUWA MAWINDO KWA MENO YAO au
kama umekamatika AUVUNJE MTEGO,
Daudi anaonyesha kuwa kutokuingia katika mtego sio kwa sababu ya ujanja wetu
bali kwa sababu ya ulinzi wa Mungu na kama umeingia katika mtego kutoka sio kwa
uwezo wako bali mtego umevunjika na mtego huo hauvunjiki wenyewe ni kwa msaada
wa Bwana, hii maana yake ni nini mwenye uwezo wa kuvunja nguvu za adui zetu ni
Mungu aliyeziumba mbingu na nchi, Ni Mungu pake yake anayeweza kukuokoa na
mauti, Ni Mungu peke yake anayeweza kukuokoa na dhambi, na ni Mungu pake yake
anayeweza kumshinda Shetani kwa niaba yetu na ni yeye anayeweza kuwa msaada kwa
nafsi zetu, na ndege akitoka mtegoni huwa harudi tena, mtegoni, Amani ya kweli
inamkalia, furaha ya moyo inarudi mzigo wa utumwa unakuwa mwepesi kwa wokovu
wake, ndege hawana mikono wanahitaji mkono wa Mungu, wanapowekwa tunduni hawawezi kutoka wenyewe mpaka mwenye huruma
awafungulie, leo mwenye huruma ataifungua nasfi yako, mwenye huruma atakuepusha
na mtego, wengine wamekamatwa na dini, wengine ulevi, wengine uraibu wa madawa
ya kukevya na ukahaba lakini yuko anayeweza kukuweka huru, popote pale ambapo
nafsi yako imeshikwa Yesu yuko tayari kukufungua.
Yohana 8:31-36 “Basi Yesu akawaambia wale
Wayahudi waliomwamini, Ninyi mkikaa katika neno langu, mmekuwa wanafunzi wangu
kweli kweli; tena mtaifahamu kweli, nayo hiyo kweli itawaweka huru. Wakamjibu,
Sisi tu uzao wake Ibrahimu, wala hatujawa watumwa wa mtu wakati wo wote; nawe
wasemaje, Mtawekwa huru? Yesu akawajibu, Amin, amin, nawaambia, Kila atendaye
dhambi ni mtumwa wa dhambi. Wala mtumwa hakai nyumbani sikuzote; mwana hukaa
sikuzote. Basi Mwana akiwaweka huru, mtakuwa huru kweli kweli.”
Mathayo 11:28-30 “Njoni kwangu, ninyi nyote
msumbukao na wenye kulemewa na mizigo, nami nitawapumzisha. Jitieni nira yangu,
mjifunze kwangu; kwa kuwa mimi ni mpole na mnyenyekevu wa moyo; nanyi mtapata
raha nafsini mwenu; kwa maana nira yangu ni laini, na mzigo wangu ni mwepesi.”
Mwandishi wa zaburi hii anaiona
kazi ya kuingilia kati na kuisaidia nafsi ya mwanadamu ni ya Mungu na ni yeye
anayestahili kuhimidiwa na kutukuzwa hakuna mwanadamu mwenye mchango wowote
katika kazi ya ukombozi wa mwanadamu zaidi ya kuokolewa kwa neema, mwanadamu ni
dhaifu sana bila Mungu, hila za shetani ziko kuishambilia nafsi ya kila mmoja
wetu ili aimeze lakini Mungu kwa rehema zake ndiye anayeweza kuuvunja mtego wa
adui zetu au kutufungulia na tukaruka zetu angani tukiwa huru kama ndege, kila
mtu aliyeokolewa anapaswa kujua wazi kuwa ni kwa neema tu na ni kwa msaada wa
Mungu tunaokolewa, Mungu amekusudia tuwe na uwanda mpana wa kuufurahia uwepo
wake na sio kufungiwa kwenye tundu kama ndege asiye na uhuru, Shetani anatumia
mitego iliyojificha kuliko mashambulizi ya wazi na ni Mungu peke yake anayeweza
kukusaidia kwanza usiingie katika mtego wa adui na kuwa mawindo, pili kama
umenaswa kuuvunja mtego ili uweze kuwa huru, Ndege hana nguvu yoyote ya kwake
ya kumsaidia kujifungulia mtego, Lakini yuko anayeweza kututunza tusiingie
mtegoni na kama umeingia anaweza kutufungulia!, Mpenzi je wewe uko katika hali
ya namna gani Umenaswa? Au unataka kunaswa? Bwana akupe neema na kukuhurumia asikuache
kuwa mawindo kwa meno yao nafsi yako iokoke kama ndege katika mtego wa wawindaji
na mtego uliokukamata uvunjike katika jina la Yesu Kristo Mwana wa Mungu aliye
hai haleluyaaaaaaaaaaa
Zaburi 124:6-8 “Na ahimidiwe Bwana;
Asiyetutoa kuwa mawindo kwa meno yao. Nafsi yetu imeokoka kama ndege Katika
mtego wa wawindaji, Mtego umevunjika, nasi tumeokoka. Msaada wetu u katika jina la Bwana,
Aliyezifanya mbingu na nchi.”
Na. Rev. Innocent Samuel Kamote
Mkuu wawajenzi mwenye Hekima


