Jumapili, 6 Septemba 2026

Nafsi yangu imeokoka kama ndege!


Zaburi 124:6-8 “Na ahimidiwe Bwana; Asiyetutoa kuwa mawindo kwa meno yao. Nafsi yetu imeokoka kama ndege Katika mtego wa wawindaji, Mtego umevunjika, nasi tumeokoka. Msaada wetu u katika jina la Bwana, Aliyezifanya mbingu na nchi.”




Utangulizi:

Ni muhimu kufahamu kuwa na hekima na maarifa yatakayokusaidia kujua namna inavyokupasa kuenenda katika ulimwengu huu wenye hila nyingi, ili uweze kujihami na kuwa salama, Katika maisha haya yenye maadui wengi!

Wakati mwingine katika maisha watakuwepo watu wenye hila, ambao kimsingi, watataka kukudhibiti, au kukuwekea mipaka katika maisha, huduma, biashara, masomo na kazi na hata kutaka kukupotezea muda kukutawala na kukukandamiza ili uwatumikie au kile kitu ambacho Mungu amekiweka ndani yako kisiweze kufanya kazi katika mazingira makuu  ya uhuru yaliyokusudiwa na Mungu au ili wewe usitoke kimaisha na ikiwezekana uendelee kuwa mtumwa wa kazi wajibu na fikra za mtawala mjanja ambaye anaweza kukunyima njia ya kujichagulia, kukunyima uhuru wa kujitegemea kuwa na maamuzi yako mwenyewe na kujiendeleza kwa sababu ya hofu yake, wivu wake au mawazo machafu hila na wao ndio wawe na maamuzi juu ya maisha yako siku zote angalia:-

Kutoka 1:8-11 “Basi akainuka mfalme mpya kutawala Misri, asiyemjua Yusufu. Akawaambia watu wake, Angalieni, watu wa wana wa Israeli ni wengi tena wana nguvu kuliko sisi. Haya! Na tuwatendee kwa akili, wasije wakaongezeka; tena, ikitokea vita, wao nao wasije wakashikamana na adui zetu na kupigana nasi, na kutoka katika nchi hii. Basi wakaweka wasimamizi juu yao wawatese kwa mizigo yao. Nao wakamjengea Farao miji ya kuwekea akiba, Pithomu na Ramesesi

Hali kama hii ndio ilikuwa sababu kubwa ya mtawala mpya katika Misri kuwaogopa Israel na kuanza kuweka mitego ya kuwadhoofisha ili ikiwezekana waweze kumezwa na wamisri na kufutika juu ya uso wa Dunia, kama sio mkono wa Mungu ulioonyooshwa na kuwatetea isingelikuwa rahisi Israel kutoka Misri, Hali hii sio stori ya Israel tu ni stori ya kila mtu amwaminiye Mungu duniani katika mikono ya adui yetu mkuu shetani na maajenti wake ambaye ndiye anataka kuitawala nafsi yako!.

Daudi na watu wake wanamshukuru Mungu kwa ukombozi wake na kwa mkono wake ulionyooshwa hata kuwapa Israel ushindi, inaonekana wazi kabisa ujanja wa adui ulikuwa wa kimkakati na wenye ulaghai mwingi sana, adui alikuwa amejipanga kuwatumikisha watu wa Mungu na  kuwabana kiasi ambacho wasingeliweza kupata msaada; mwenyewe anaona mpango wa adui ulikuwa ni kuwameza wakiwa hai, Kumezwa ukiwa hai ni kuchukuliwa mateka na kunyimwa uhuru wako huku ukiteswa nafsi yako  na kutumikishwa  ukiwa umefungwa kabisa kiasi ambacho ni mpaka usaidiwe na mtu wa nje hivi ndivyo adui alivyokuwa amemkusudia Daudi na jamii yake iliyokuwa ikimzunguka. Ona:-

Zaburi 124:1-5 “Kama si Bwana aliyekuwa pamoja nasi, Israeli na aseme sasa, Kama si Bwana aliyekuwa pamoja nasi, Wanadamu walipotushambulia. Papo hapo wangalitumeza hai, Hasira yao ilipowaka juu yetu Papo hapo maji yangalitugharikisha, Mto ungalipita juu ya roho zetu; Papo hapo yangalipita juu ya nafsi zetu Maji yafurikayo

Daudi anaizungumzia hali iliyoikuta nafsi yake na jamii yake sawa na ndege aliyetegewa mtego kisha akakamatika na kuwekwa tunduni, ndege huyu angekosa uhuru wake na maamuzi yake na angetawaliwa maisha yake yangekuwa chini ya amri ya aliyemkamata na kumwekea mtego tu, kama ndege asiyekuwa na nguvu katika mikono ya utawala wa watega mitego isingekuwa rahisi kupata ukombozi mpaka mtu mwenye nguvu zaidi aje akukomboe, Kwa hiyo Daudi na wenzake wanauona wokovu walioupata kuwa sio swala la kubahatisha  bali ni tendo la Mungu mwenye nguvu kuingilia kati na kuivunja mitego ya adui na ndipo nafsi zao zikaokoka na ndio maana katika Zaburi hii anamhimidi Bwana ambaye alizuia kwa namna zote wao kuwa mawindo ya adui na kuwaokoa:-

Wakolosai 1:13-14 “Naye alituokoa katika nguvu za giza, akatuhamisha na kutuingiza katika ufalme wa Mwana wa pendo lake; ambaye katika yeye tuna ukombozi, yaani, msamaha wa dhambi;”

Leo katika mpango wa Mungu tutachukua muda kujifunza somo hili “Nafsi yangu imeokoka kama ndege” kwa kuzingatia vipengele vitatu muhimu vifuatavyo:-

 

·         Ndege katika mtego wa wawindaji.

·         Nafsi katika mitego ya wawindaji.

·         Nafsi yangu imeokoka kama ndege.

 

Ndege katika mtego wa wawindaji.

Zaburi 124:6-8 “Na ahimidiwe Bwana; Asiyetutoa kuwa mawindo kwa meno yao. Nafsi yetu imeokoka kama ndege Katika mtego wa wawindaji, Mtego umevunjika, nasi tumeokoka.  Msaada wetu u katika jina la Bwana, Aliyezifanya mbingu na nchi.”

Ni muhimu kufahamu kuwa kama kuna viumbe wameumbwa wakiwa na uhuru wa asili, basi Ndege ni kiumbe aliyeumbwa akiwa na uhuru huo wa asili, wana uhuru wa asili na mpana sana waliopewa na Mungu, lakini sio hivyo tu ni viumbe ambao Mungu anawajali kiasi kwamba hawana hofu ya maisha, Mungu mwenyewe anawalisha na kuwatunza kwa kiwango cha ajabu sana, Ndege wana ulinzi wa ajabu sana kwa mujibu wa Biblia hakuna ndege anayeanguka bila mbingu kuwa na taarifa, kwa hiyo ndege ni kiumbe chenye ulinzi wa ajabu kutoka kwa Mungu.

Mwanzo 1:20-22 “Mungu akasema, Maji na yajawe kwa wingi na kitu kiendacho chenye uhai, na ndege waruke juu ya nchi katika anga la mbingu. Mungu akaumba nyangumi wakubwa, na kila kiumbe chenye uhai kiendacho, ambavyo maji yalijawa navyo kwa wingi kwa jinsi zao, na kila ndege arukaye, kwa jinsi yake; Mungu akaona ya kuwa ni vyema. Mungu akavibarikia, akisema, Zaeni, mkaongezeke, mkayajaze maji ya baharini, ndege na wazidi katika nchi.”

Mathayo 6:25-26 “Kwa sababu hiyo nawaambieni, Msisumbukie maisha yenu, mle nini au mnywe nini; wala miili yenu, mvae nini. Maisha je! Si zaidi ya chakula, na mwili zaidi ya mavazi? Waangalieni ndege wa angani, ya kwamba hawapandi, wala hawavuni, wala hawakusanyi ghalani; na Baba yenu wa mbinguni huwalisha hao. Ninyi je! Si bora kupita hao?

Mathayo 10:28-31 “Msiwaogope wauuao mwili, wasiweze kuiua na roho; afadhali mwogopeni yule awezaye kuangamiza mwili na roho pia katika jehanum. Je! Mashomoro wawili hawauzwi kwa senti moja? Wala hata mmoja haanguki chini asipojua Baba yenu; lakini ninyi, hata nywele za vichwa vyenu zimehesabiwa zote. Msiogope basi; bora ninyi kuliko mashomoro wengi.”

Unaona Mungu amewaumba ndege wawe na uhuru mpana wa asili, waitamalaki dunia vyovyote wapendavyo, Ndege wanatunzwa na Mungu, hawaangaiki kulima wala kuweka ghalani, lakini Mungu anawalisha, wana furaha wana amani, lakini zaidi ya yote Mungu anawajali kiasi ambacho hawaanguki chini bila mbingu kuwa na taarifa, Lakini changamoto kubwa ya ndege ni wawindaji, Mwanadamu ni kiumbe wa maana zaidi kuliko ndege, Mungu anamjali mwanadamu katika namna isiyoweza kuelezeka Mwandishi mmoja mpka akamuhoji Mungu, Mtu ni kitu gani hata umwangalie

Hata hivyo adui mkubwa wa mwanadamu ni mwanadamu, Mwanadamu ambaye wakati wewe ukiwa huna madhara kwa mtu wala huwazii mabaya juu ya mtu, wawindaji wanakuwazia mabaya na wanataka kuitega nafsi yako, Ndege ni kiumbe dhaifu sana na kuna watu wanataka kumkamata ili wamweke katika tundu, hapo wanataka ndege awe na uhuru finyu, na walimshe wao badala ya Mungu, huu ndio mkakati wa shetani, yeye anataka kuikamata nafsi yako, aifunge akutumikishe usifurahie ule uhuru na maisha uliyopewa na Mungu, leo hata kama nasfi yako imekamatika ninakutangazia kuwa ni siku ya kwenda kuzifungulia nasfi zilizofungwa na kuwekewa mipaka katika jina la Yesu Kristo mwana wa Mungu aliye hai.

Wawindaji sio watu wazuri hata kidogo, wao mpango wao ni kuikamata nafsi yako, na hili ndilo jangwa kubwa sana la kiroho hapa duniani  yaani pale nafsi yako inapokuwa imekamatika, Maandiko yanaonyesha kuwa mtu akifanikiwa kuiteka nafsi yako hususani kama ni adui anaweza kukuweka katika hali ya hatari kubwa sana na kusababisha uharibifu mkubwa wa kiroho na kuitishia usalama wako na kukukosesha amani katika maisha, Waandishi wa Zaburi mara kwa mara wameonyesha kuwa adui anaziwinda nafsi zetu na ili uweze kupata msaada kama umekamatika au unawindwa basi ni Mungu peke yake  ndiye anayeweza kukusaidia na kukuokoa na kuirejesha nafsi yako katika uhuru wake ona:-

Zaburi 7:1-2 “Bwana, Mungu wangu, nimekukimbilia Wewe, Uniokoe na wote wanaonifuatia, uniponye. Asije akaipapura nafsi yangu kama simba, Akiivunja-vunja pasipokuwa na wa kuponya.”

Zaburi 59:1-3 “Ee Mungu wangu, uniponye na adui zangu, Uniinue juu yao wanaoshindana nami. Uniponye nao wafanyao maovu, Uniokoe na watu wa damu. Kwa maana wanaiotea nafsi yangu; Wenye nguvu wamenikusanyikia; Ee Bwana, si kwa kosa langu, Wala si kwa hatia yangu.”

Mwandishi wa Zaburi hii Daudi anazungumza kwa lugha ya fumbo au lugha ya kimashairi akilinganisha maisha yake au nafsi yake kama maisha ya ndege, Ndege ni viumbe dhaifu sana na hawana nguvu ya kujitetea  na wala wengi hawajui kama wanawindwa au wana maadui, moyo wa ndege wengi ni moyo mwororo na mnyoofu ndege hawana neno na mtu wao wanapoamka asubuhi hawafikiri kufanya uadui na mtu, wao huamka na kumtukuza Mungu kisha kuendelea na majukumu yao ya kila siku, hawajui kama kuna mtu ataamka na kuwawekea mtego, wala hawajui kuwa kuna mtu ataamka na kuwageuza wao kuwa mfugo au kitoweo au kuwafungua katika tundu hawajui kama kuna wawindaji, ni muhimu ukaishi maisha yako lakini uwe makini na wawindaji, wawindaji wako kila mahali!

Lugha hii anayoitumia mwandishi wa Zaburi inawahusu watu wanaomcha Mungu, wengi wanawindwa nafsi zao lakini hawajui, wengi huamini kila mtu na wakati mwingine hawajui kama kuna mtu anaweza kuwa adui na kuziwinda nafsi zao, Ndege anawakilisha udhaifu wa mwanadamu, Hakuna mwanadamu mwenye nguvu ya kuvunja mitego ya adui Shetani na hata kujiokoa katika mikono yake, Shetani hutumia njia mbalimbali katika kuhakikisha kuwa unaingia kwenye mitego yake ikiwa ni pamoja na kuitumia hofu, magonjwa, dhambi, mauti,  na mashambulizi makali kutoka kwa majeshi yake ya pepo wabaya na watumishi wake wanadamu yaani maajenti wake, waganga, wachawi,  wanga, wenye hila na wenye wivu,Tunapoishi duniani fahamu na kuelewa kuwa wewe ni dhaifu kama ndege na bila masaada wa Mungu ni vigumu kwako kuwa huru kama Mungu mwenye nguvu hatakulinda na kukuepusha na mitego ya wawindaji, kila kitu duniani ulicho nacho kinawindwa, wewe hujui, ndoa yako inawindwa, kazi yako inawindwa, cheo chako kinawindwa, mali zako zinawindwa, biashara yako inawindwa, familia yako inawindwa, masomoni, unawindwa, huduma yako inawindwa, wawindaji ni watu wenye uchungu, ni wenye wivu, ni wenye nia mbaya, ni wenye hila na wamejaa kila mahali duniani, hata kwenye genge lako la nyanya pale sokoni, unawindwa, kama ndege katika mtego wa wawindaji, Bwana akupe neema kuigundua mitego yote unayotegewa na akuokoe na mitego ya wawaindaji katika jina la Yesu Kristo sema ameeeen!

Nafsi katika mitego ya wawindaji

Tumeona kuwa maisha ya mwanadamu ni kama maisha ya ndege katika mitego ya adui, na kinachowindwa katika maisha yetu mara tu baada ya kuzaliwa kwetu ni Nafsi, Neno nafsi katila lugha ya kiebrania ni “Nephesh” ambalo linamaanisha uhai, nafsi au mtu wa ndani, mwanadamu ana sehemu kuu tatu Mwili, Nafsi na Roho, vita vyetu vyote vya kiroho na kimaamuzi vinafanyika katika nafsi, nafsi inaponaswa katika mtego ambao unajulikana kama “Pach” Kiebrania ikimaanisha “tanzi”, au mbinu za kunasia, na wawindaji wanaitwa “Yagosh” Kiebrania yaani  watu wenye hila au wanasao kwa hila, wenye wivu, wenye uchungu, wasiopenda maendeleo yako, sasa nafsi inapokamatwa unaingizwa katika utumwa wa mwindaji na huwezi kuachiwa mpaka Mungu aingilie kati, mtu anapokuendea kwa mganga kukuroga maana yake anaitafuta nafsi yako aikamate na kuielekeza kule anakotaka yeye, nafsi yako ikikamatwa unaingia utumwani unamezwa ukiwa hai unapoteza uhuru uliokusudiwa na Mungu katika maisha yako!, unaona maisha yako ni kama yako gizani nafsi yako imekalishwa mahali penye giza, watu wamekufunga, umekuwa kama ndege katika tundu unafugwa badala ya kuwa na uhuru wako mpana wa asili uliokusudiwa na Mungu!

Zaburi 143:3-4 “Maana adui ameifuatia nafsi yangu, Ameutupa chini uzima wangu. Amenikalisha mahali penye giza, Kama watu waliokufa zamani. Na roho yangu imezimia ndani yangu, Moyo wangu ndani yangu umesituka.”

Adui wanapoipata nafsi yako kila kitu ndani yako na mali yako kinachukuliwa mateka na nafsi yako ndiyo inayoteseka, na maisha yako yanaharibiwa unatupwa chini, unawekwa kwenye giza na unakuwepo duniani lakini ni kama mtu aliyekufa, wawindaji wakiishika nafsi yako wanajivunia majivumo makubwa wanatamba kuwa wamekuweza na huwezi kufurukuta tena, wamekuweka kwenye kiganja, wokovu wako au ukombozi wako ni mpaka Bwana pekee aingilie kati, nafsi ikishikwa unakuwa mtumwa huwezi kufanya unalotaka wala huwezi kufanya mapenzi ya Mungu bali utafanya kile nafsi yako inakokukokota na adui zako wanakokupeleka, utasikia yule sisi tumemuweka kwenye kiganja ujue wameishika nafsi yako, Utasikia Bosi mimi haniambii kitu nimemuweka hapa! ahaa nafsi imeshikwa, Makahaba wanaoiba waume za watu huwa wanatafuta kuwashika nafsi, wakishawashika, mumeo harudi kwako kwa watai, fedha anapeleka huko, anapewa raha za ajabu na kupikiwa vizuri ili wewe usahau familia yako na umtese mkeo wako kwa nini changamoto nafsi ikishatekwa umetekwa maisha yako yote, ukitaka kumtumikisha mtu mshike nafsi yake, watu wengi wameshikwa na wanatumika wakati mwingine bila kupenda!

Farao alipowakamata Israel na kuwaweka kwenye tundu la utumwa nani angeweza kuwafungulia? Ni mpaka mwenye nguvu alipoingilia kati na kushughulika na adui ndipo Bwana alipowaweka huru! Ona  

Kutoka 15:6-13 “BWANA, mkono wako wa kuume umepata fahari ya uwezo, BWANA, mkono wako wa kuume wawaseta-seta adui. Kwa wingi wa ukuu wako wawaangusha chini wanaokuondokea, Wapeleka hasira yako, nayo huwateketeza kama mabua makavu. Kwa upepo wa mianzi ya pua yako maji yalipandishwa, Mawimbi yakasimama juu wima mfano wa chungu, Vilindi vikagandamana ndani ya moyo wa bahari. Adui akasema, Nitafuatia, nitapata, nitagawanya nyara, Nafsi yangu itashibishwa na wao; Nitaufuta upanga wangu, mkono wangu utawaangamiza. Ulivuma kwa upepo wako, bahari ikawafunikiza; Wakazama kama risasi ndani ya maji makuu. Ee BWANA, katika miungu ni nani aliye kama wewe? Ni nani aliye kama wewe, mtukufu katika utakatifu, Mwenye kuogopwa katika sifa zako, mfanya maajabu? Ulinyosha mkono wako wa kuume, Nchi ikawameza. Wewe kwa rehema zako umewaongoza watu uliowakomboa, Kwa uweza wako uliwaelekeza hata makao yako matakatifu

Unaona Israel waliposhikwa ni Bwana ndiye aliyekuja kuwatoa, leo ni siku ambayo kila ambaye ameshikilia nafsi yako anaiachia kwa mkono wa Bwana ulio hodari ulioonyooshwa katika jina la Yesu!

Nafsi yangu imeokoka kama ndege

Zaburi 124:6-8 “Na ahimidiwe Bwana; Asiyetutoa kuwa mawindo kwa meno yao. Nafsi yetu imeokoka kama ndege Katika mtego wa wawindaji, Mtego umevunjika, nasi tumeokoka.  Msaada wetu u katika jina la Bwana, Aliyezifanya mbingu na nchi.”

Mwandishi anaijua historia na mbinu ya adui kuwa anachikotafuta ni nafsi na anaelewa wazi kuwa nafsi inawindwa kama ndege na kuwa wenye hila huweka mitego yao ili kutunasa kama ndege na wokovu wako unaweza kuja kwa namna mbili aidha Mungu akuokoe usiwe mawindo, ASIYETUTOA KUWA MAWINDO KWA MENO YAO au kama umekamatika AUVUNJE MTEGO, Daudi anaonyesha kuwa kutokuingia katika mtego sio kwa sababu ya ujanja wetu bali kwa sababu ya ulinzi wa Mungu na kama umeingia katika mtego kutoka sio kwa uwezo wako bali mtego umevunjika na mtego huo hauvunjiki wenyewe ni kwa msaada wa Bwana, hii maana yake ni nini mwenye uwezo wa kuvunja nguvu za adui zetu ni Mungu aliyeziumba mbingu na nchi, Ni Mungu pake yake anayeweza kukuokoa na mauti, Ni Mungu peke yake anayeweza kukuokoa na dhambi, na ni Mungu pake yake anayeweza kumshinda Shetani kwa niaba yetu na ni yeye anayeweza kuwa msaada kwa nafsi zetu, na ndege akitoka mtegoni huwa harudi tena, mtegoni, Amani ya kweli inamkalia, furaha ya moyo inarudi mzigo wa utumwa unakuwa mwepesi kwa wokovu wake, ndege hawana mikono wanahitaji mkono wa Mungu, wanapowekwa tunduni hawawezi kutoka wenyewe mpaka mwenye huruma awafungulie, leo mwenye huruma ataifungua nasfi yako, mwenye huruma atakuepusha na mtego, wengine wamekamatwa na dini, wengine ulevi, wengine uraibu wa madawa ya kukevya na ukahaba lakini yuko anayeweza kukuweka huru, popote pale ambapo nafsi yako imeshikwa Yesu yuko tayari kukufungua.

Yohana 8:31-36 “Basi Yesu akawaambia wale Wayahudi waliomwamini, Ninyi mkikaa katika neno langu, mmekuwa wanafunzi wangu kweli kweli; tena mtaifahamu kweli, nayo hiyo kweli itawaweka huru. Wakamjibu, Sisi tu uzao wake Ibrahimu, wala hatujawa watumwa wa mtu wakati wo wote; nawe wasemaje, Mtawekwa huru? Yesu akawajibu, Amin, amin, nawaambia, Kila atendaye dhambi ni mtumwa wa dhambi. Wala mtumwa hakai nyumbani sikuzote; mwana hukaa sikuzote. Basi Mwana akiwaweka huru, mtakuwa huru kweli kweli.

Mathayo 11:28-30 “Njoni kwangu, ninyi nyote msumbukao na wenye kulemewa na mizigo, nami nitawapumzisha. Jitieni nira yangu, mjifunze kwangu; kwa kuwa mimi ni mpole na mnyenyekevu wa moyo; nanyi mtapata raha nafsini mwenu; kwa maana nira yangu ni laini, na mzigo wangu ni mwepesi.”

Mwandishi wa zaburi hii anaiona kazi ya kuingilia kati na kuisaidia nafsi ya mwanadamu ni ya Mungu na ni yeye anayestahili kuhimidiwa na kutukuzwa hakuna mwanadamu mwenye mchango wowote katika kazi ya ukombozi wa mwanadamu zaidi ya kuokolewa kwa neema, mwanadamu ni dhaifu sana bila Mungu, hila za shetani ziko kuishambilia nafsi ya kila mmoja wetu ili aimeze lakini Mungu kwa rehema zake ndiye anayeweza kuuvunja mtego wa adui zetu au kutufungulia na tukaruka zetu angani tukiwa huru kama ndege, kila mtu aliyeokolewa anapaswa kujua wazi kuwa ni kwa neema tu na ni kwa msaada wa Mungu tunaokolewa, Mungu amekusudia tuwe na uwanda mpana wa kuufurahia uwepo wake na sio kufungiwa kwenye tundu kama ndege asiye na uhuru, Shetani anatumia mitego iliyojificha kuliko mashambulizi ya wazi na ni Mungu peke yake anayeweza kukusaidia kwanza usiingie katika mtego wa adui na kuwa mawindo, pili kama umenaswa kuuvunja mtego ili uweze kuwa huru, Ndege hana nguvu yoyote ya kwake ya kumsaidia kujifungulia mtego, Lakini yuko anayeweza kututunza tusiingie mtegoni na kama umeingia anaweza kutufungulia!, Mpenzi je wewe uko katika hali ya namna gani Umenaswa? Au unataka kunaswa? Bwana akupe neema na kukuhurumia asikuache kuwa mawindo kwa meno yao nafsi yako iokoke kama ndege katika mtego wa wawindaji na mtego uliokukamata uvunjike katika jina la Yesu Kristo Mwana wa Mungu aliye hai haleluyaaaaaaaaaaa

Zaburi 124:6-8 “Na ahimidiwe Bwana; Asiyetutoa kuwa mawindo kwa meno yao. Nafsi yetu imeokoka kama ndege Katika mtego wa wawindaji, Mtego umevunjika, nasi tumeokoka.  Msaada wetu u katika jina la Bwana, Aliyezifanya mbingu na nchi.”

 

Na. Rev. Innocent Samuel Kamote

Mkuu wawajenzi mwenye Hekima

Jumapili, 30 Agosti 2026

Huduma ya watoto


Waamuzi 2:8-13 “Kisha Yoshua mwana wa Nuni, mtumishi wa Bwana, akafa, naye alipata umri wa miaka mia na kumi. Nao wakamzika katika mpaka wa urithi wake katika Timnath-heresi, katika nchi ya vilima vilima ya Efraimu, upande wa kaskazini wa mlima wa Gaashi.Tena watu wote wa kizazi hicho nao walikusanywa waende kwa baba zao; kikainuka kizazi kingine nyuma yao, ambacho hakikumjua Bwana, wala hawakuijua hiyo kazi ambayo alikuwa ameitenda kwa ajili ya Israeli. Wana wa Israeli walifanya yaliyokuwa ni maovu mbele za macho ya Bwana, nao wakawatumikia Mabaali. Wakamwacha Bwana, Mungu wa baba zao, aliyewaleta kutoka katika nchi ya Misri, wakafuata miungu mingine, baadhi ya miungu ya watu wale waliokaa karibu nao pande zote, wakajiinamisha mbele yao; wakamkasirisha Bwana, akaghadhibika. Wakamwacha Bwana, wakamtumikia Baali na Maashtorethi.”




Utangulizi:

Mojawapo ya jukumu kubwa la Kanisa pamoja na mambo mengine ni pamoja na kuwahudumia watoto, Mungu amewapa watoto kipuambele kikubwa sana na kwa sababu hiyo kuwapuuzia watoto ni kumpuuzia Mungu, Kanisa lina wajibu wa kuwajenga na kuwahudumia watoto kwa uaminifu vilevile kama linavyowahudumia watu wazima iko dhana potofu kwa wahudumu wengi wa injili inayofikiri kuwapuuzia watoto na kutokutaka kuwaleta karibu na Yesu kufanya hivi ni kufanya makosa makubwa sana ambayo Yesu mwenyewe aliyakemea.

Mathayo 19:13-15 “Ndipo akaletewa watoto wadogo ili aweke mikono yake juu yao na kuwaombea; wanafunzi wake wakawakemea. Lakini Yesu akasema, Waacheni watoto wadogo waje kwangu; wala msiwazuie; kwa maana walio mfano wa hao, ufalme wa mbinguni ni wao. Akaweka mikono yake juu yao, akatoka huko.” 

Kama tunamtumikia Mungu kwa haki na kweli na kama tunatanguliza maslahi ya ufalme wa mbinguni basi hatutaweza kamwe kuwaacha nyuma watoto katika mambo ya Mungu ni lazima twende pamoja na wao na kuwakuza katika neema hii kwani malezi ya wototo wadogo katika njia ya Mungu ni maagizo ya kibiblia Mithali 22:6 “Mlee mtoto katika njia impasayo, Naye hataiacha, hata atakapokuwa mzee.”

Kumbukumbu 6:4-9 “Sikiza, Ee Israeli; Bwana, Mungu wetu, Bwana ndiye mmoja. Nawe mpende Bwana, Mungu wako, kwa moyo wako wote, na kwa roho yako yote, na kwa nguvu zako zote. Na maneno haya ninayokuamuru leo, yatakuwa katika moyo wako; nawe uwafundishe watoto wako kwa bidii, na kuyanena uketipo katika nyumba yako, na utembeapo njiani, na ulalapo, na uondokapo. Yafunge yawe dalili juu ya mkono wako, nayo yatakuwa kama utepe katikati ya macho yako.Tena yaandike juu ya miimo ya nyumba yako, na juu ya malango yako.”

Kwa msingi huo wakati huu sisi kama watendakazi na wahudumu katika shamba la Mungu tutachua muda kujifunza kwa kina na mapana na marefu kuhusiana na swala zima la huduma ya watoto kwa kuzingatia vipengele vitatu muhimu vifuatavyo:-

  • Umuhimu wa huduma ya watoto
  • Umuhimu wa walimu wa watoto
  • Jinsi ya kufanikisha huduma ya watoto

 

Umuhimu wa huduma ya watoto

Tumeona katika utangulizi wa somo hili jinsi Mungu alivyowapa watoto kipaumbele watoto, Mungu anataka watoto wajulishwe njia zake, aliwaamuru Israel kufanya hivyo na kwakweli wao wamekuwa hodari katika kuhakikisha kuwa watoto wao wanafuata njia zao na imani yao, sisi nasi kama Kanisa hatuna budi kulishika hili vile vile na kuhakikisha kuwa hatuwaachi watoto wetu bila ujuzi wa neno la Mungu ili wakue katika njia hii na imani hii

Zaburi 78:5-7 “Maana alikaza ushuhuda katika Yakobo, Na sheria aliiweka katika Israeli. Aliyowaamuru baba zetu Wawajulishe wana wao, Ili kizazi kingine wawe na habari, Ndio hao wana watakaozaliwa. Wasimame na kuwaambia wana wao Wamwekee Mungu tumaini lao. Wala wasiyasahau matendo ya Mungu, Bali wazishike amri zake.”

Mungu anaeleza baadae siri ni kwanini alimchagua Abrahamu, Mungu anasema alimjua Abrahamu kwamba atawafundisha watoto wake waishike njia yake baada yake na kuwaamuru kutenda haki, Kumbe basi Mungu anapogundua kuwa tumemaanisha katika kuwahudumia watoto na washirika kwa ujumla atatufurahia na kuruhusu maelfu ya watu wake waje kwetu akijua ya kuwa watoto watafundishwa njia za Mungu katika Kanisa letu, Kanisa linalowajali watoto Mungu hulibariki sana!

Mwanzo 18:18-19 “BWANA akanena, Je! Nimfiche Ibrahimu jambo nilifanyalo, akiwa Ibrahimu atakuwa taifa kuu, hodari, na katika yeye mataifa yote ya dunia watabarikiwa? Kwa maana nimemjua ya kwamba atawaamuru wanawe, na nyumba yake baada yake waishike njia ya BWANA, wafanye haki na hukumu, ili kwamba BWANA naye akamtimizie Ibrahimu ahadi zake.”

Huduma ya watoto ni kazi maalumu ya kuujenga ufalme wa Mungu, hii sio huduma ya malezi ya kuwatunza watoto wakati wazazi wanasali au wako katika ibada, hii ni huduma maalumu ya kumjenga mtoto kiroho, kimaadili na kitabia, kwa kuushika moyo wake mapema na kumfundisha njia za Mungu katika hatua za awali kwa lugha, mbinu na njia zitakazowafanya watoto kuelewa kwa haraka Mithali 22:6 “Mlee mtoto katika njia impasayo, Naye hataiacha, hata atakapokuwa mzee.”

Endapo kanisa litaacha wajibu huu muhimu na kuwaacha watenda kazi wake, wanafunzi, wahudumu na wenye hekima wakiwa hawana ujuzi kuhusu maswala ya watotoni Dhahiri kuwa tunaandaa kizazi ambacho hakitakuwa kinamjua Mungu kama kile kilichoinuka nyakati za wazee wetu katika Israel baada ya kufa kwake Yoshua na wakati wa kizazi cha nyakati za waamuzi ambao walicheza sana na mambo ya hvyo na kuwapa adui zao nafasi ya kuwaonea na kuwakandamiza

Waamuzi 2:8-12 “Kisha Yoshua mwana wa Nuni, mtumishi wa Bwana, akafa, naye alipata umri wa miaka mia na kumi. Nao wakamzika katika mpaka wa urithi wake katika Timnath-heresi, katika nchi ya vilima vilima ya Efraimu, upande wa kaskazini wa mlima wa Gaashi. Tena watu wote wa kizazi hicho nao walikusanywa waende kwa baba zao; kikainuka kizazi kingine nyuma yao, ambacho hakikumjua Bwana, wala hawakuijua hiyo kazi ambayo alikuwa ameitenda kwa ajili ya Israeli. Wana wa Israeli walifanya yaliyokuwa ni maovu mbele za macho ya Bwana, nao wakawatumikia Mabaali.Wakamwacha Bwana, Mungu wa baba zao, aliyewaleta kutoka katika nchi ya Misri, wakafuata miungu mingine, baadhi ya miungu ya watu wale waliokaa karibu nao pande zote, wakajiinamisha mbele yao; wakamkasirisha Bwana, akaghadhibika.”

Mungu atupe neema na hekima kizazi cha leo, tusipuuzie swala hili nyeti linalohusiana na huduma hii ya watoto ili kwa upendo na kwa masalahi ya ufalme wa Mungu tusimtengenezee Bwana kizazi au Kanisa la baadae lisilomjua Mungu wala njia zake kwani kwa kufanya hivyo tutakuwa tunamkosea Bwana hivyo huduma hii ya kuwafudnisha watoto njia za Bwana ni mapenzi yake, kumbuka neno la Msingi Kikainuka kizazi kingine hapo maana yake ni kizazi kilichokosa mafundisho, kizazi kisichorithishwa imani, kizazi kilichokosa uangalizi wa kiroho, kizazi ambacho hakuna mtu anakijali, kizazi ambacho hata stori kuhusu Mungu na matendo yake makuu hawakuwahi kuyasikia. 


Umuhimu wa walimu wa watoto

Wahudumu wanaohusika na kuwafundisha watoto wanapaswa kuwa na uelewa wa kina kuwa wao ni wa muhimu sana kuliko mtu yeyote yule kwa sababu wao ndio wanaouweka msingi wa mwanzo kabisa wa imani kwa watoto, wanaipanda mbegu ya imani na uadilifu na kuwajengea watoto tabia njema na kuwafunda ili wakue na kuwa kama Yesu katika upendo, imani mwenendo na usafi, wanalazimika kujikoki na kufanya maandalizi ya kutosha na ya kina ili kuboresha mwenendo mzima wa malezi elekezi  kwa watoto hawa, kwa kufanya hivi wao wanaandaa kile kizazi kijacho cha watu waliofunzwa na wenye nidhamu ya hali ya juu watakaokuwa nuru na chumvi kwa ulimwengu ujao.

-          Wao ni wajenzi wa msingi na ukuaji bora wa watoto kiroho, wanawasaidia watoto kukua wakiwa imara kiimani na kuhakikisha kuwa msingi huo unadumu siku zote za maisha yao, hapo tunawatengenezea uwezo wa kusikia na kulitendea kazi neno la Mungu jambo litakalowafanya wakue wakiwa imara  na wenye ujuzi kuhusu Mungu.

 

Luka 6:47-49 “Kila mtu ajaye kwangu, na kuyasikia maneno yangu na kuyatenda, nitawaonyesha mfano wake. Mfano wake ni mtu ajengaye nyumba, na kuchimba chini sana, na kuweka msingi juu ya mwamba; na kulipokuja gharika, mto uliishukia nyumba ile kwa nguvu, usiweze kuitikisa; kwa kuwa imejengwa vizuri. Lakini yule aliyesikia ila hakutenda, mfano wake ni mtu aliyejenga nyumba juu ya ardhi pasipokuwa na msingi, mto ukaishukia kwa nguvu, ikaanguka mara; na maangamizi yake nyumba ile yakawa makubwa.”

 

-          Wao ni warithishaji wa mila na tamaduni za kiimani (Pedagogies) walimu wa watoto katika Kanisa wanafanya kazi ya kuwaandaa wana wa kifalme kusimama imara na kuwa hodari katika  maneno na matendo ya kazi zao za kifalme, Nyakati za Biblia watoto wa kifalme walikuwa na waalimu wao ambao kazi zao zilikuwa ni ni kuwafundisha watoto wa kifalme kwa kuwarithisha mila miiko na desturi za kifalme ili watakapokuja kuwa wafalme wasikiuke mila na desturi hizo, wakiwa na uwezo wa kusema na kutenda, au kufundisha na kufanya.

 

Matendo 1:1 “Kitabu kile cha kwanza nalikiandika, Theofilo, katika habari ya mambo yote aliyoanza Yesu kufanya na kufundisha,”

 

Matendo 7:22 “Musa akafundishwa hekima yote ya Wamisri, akawa hodari wa maneno na matendo.”

 

-          Wao ni wawezeshaji wa kusikia na kutenda  Msingi mkubwa sana wa walimu wa neno la Mungu unakazia katika kusikia na kutenda, kimsingi kama mtu hajatenda kibiblia humaanisha hajasikia, Mwalimu mzuri na mwema ni yule aneyewawezesha watoto kusikia kisha wakatenda huu ndio mkazo wa waalimu wa kibiblia na ndicho wanacho paswa kukifanya walimu wa watoto.

 

Mathayo 7:24-27 “Basi kila asikiaye hayo maneno yangu, na kuyafanya, atafananishwa na mtu mwenye akili, aliyejenga nyumba yake juu ya mwamba; mvua ikanyesha, mafuriko yakaja, pepo zikavuma, zikaipiga nyumba ile, isianguke; kwa maana misingi yake imewekwa juu ya mwamba.Na kila asikiaye hayo maneno yangu asiyafanye, atafananishwa na mtu mpumbavu, aliyejenga nyumba yake juu ya mchanga; mvua ikanyesha, mafuriko yakaja, pepo zikavuma, zikaipiga nyumba ile, ikaanguka; nalo anguko lake likawa kubwa.

 

Yakobo 1:22-25 “Lakini iweni watendaji wa neno, wala si wasikiaji tu, hali mkijidanganya nafsi zenu. Kwa sababu mtu akiwa ni msikiaji wa neno tu, wala si mtendaji, mtu huyo ni kama mtu anayejiangalia uso wake katika kioo. Maana hujiangalia, kisha huenda zake, mara akasahau jinsi alivyo. Lakini aliyeitazama sheria kamilifu iliyo ya uhuru, na kukaa humo, asiwe msikiaji msahaulifu, bali mtendaji wa kazi, huyo atakuwa heri katika kutenda kwake.”

 

Mathayo 21:28-32 “Lakini mwaonaje? Mtu mmoja alikuwa na wana wawili; akamwendea yule wa kwanza, akasema, Mwanangu, leo nenda kafanye kazi katika shamba la mizabibu. Akajibu akasema, Naenda, Bwana; asiende. Akamwendea yule wa pili, akasema vile vile. Naye akajibu akasema, Sitaki; baadaye akatubu, akaenda. Je! Katika hao wawili ni yupi aliyefanya mapenzi ya babaye? Wakamwambia, Ni yule wa pili. Basi Yesu akawaambia, Amin nawaambia, watoza ushuru na makahaba wanatangulia mbele yenu kuingia katika ufalme wa Mungu. Kwa sababu Yohana alikuja kwenu kwa njia ya haki, ninyi msimwamini; lakini watoza ushuru na makahaba walimwamini, nanyi hata mlipoona, hamkutubu baadaye, ili kumwamini.”

 

-          Wao ni chachu ya makuzi ya kiroho Msingi wa ukuaji wa kiroho, kumpenda Mungu na kumtumikia ni mchakato wa muda mrefu sana unaojumuisha toba, maendeleo ya kukua kiroho, kiimani na kimafundisho, ili mtoto akue akimpendeza Mungu na wanadamu anapaswa kuwa na walimu bora wanaojua wanampeleka wapi mtoto, wao wenyewe wakiwa ndio kielelezo cha ibada, heshima na utumishi, Kanisa hatuna budi kuwekeza katika mioyo ya watoto kwa mafundisho sahihi, tuwalishe kondoo wa Mungu bila kujali umri wao au kuwapuuzia.

 

Yohana 21:15 “Basi walipokwisha kula, Yesu akamwambia Simoni Petro, Je! Simoni wa Yohana, wewe wanipenda kuliko hawa? Akamwambia, Naam, Bwana, wewe wajua kuwa nakupenda. Akamwambia, Lisha wana-kondoo wangu. Akamwambia tena mara ya pili, Simoni wa Yohana, wanipenda? Akamwambia, Ndiyo, Bwana, wewe wajua kuwa nakupenda. Akamwambia, Chunga kondoo zangu. Akamwambia mara ya tatu, Simoni wa Yohana, wanipenda? Petro alihuzunika kwa vile alivyomwambia mara ya tatu, Wanipenda? Akamwambia, Bwana, wewe wajua yote; wewe umetambua ya kuwa nakupenda. Yesu akamwambia, Lisha kondoo zangu.”

 

-           Wao huwajengea tabia njema mapema – walimu wa watoto ndio wanaopanda msingi wa tabia njema mapema, na hata mtu anapokuja kuwa mtu mzima kimsingi mambo mengi sana yanakuwa yamejengeka tangu utoto, Bibi yake Timotheo na mama yake licha ya kuwa wazazi lakini pia walikuwa walimu wa awali wa Imani safi isiyo na unafiki wakiipandikiza hivyo kwa Timotheo na kumfanya Timitheo kuja kuwa mtu mwenye sifa njema sana miongoni mwa wanafunzi wa nyakati za kanisa la kwanza, vigezi vulivyomfanya Paulo aambatane naye.

 

2Timotheo 3:13-15. “lakini watu wabaya na wadanganyaji wataendelea, na kuzidi kuwa waovu, wakidanganya na kudanganyika. Bali wewe ukae katika mambo yale uliyofundishwa na kuhakikishwa, kwa maana unajua ni akina nani ambao ulijifunza kwao; na ya kuwa tangu utoto umeyajua maandiko matakatifu, ambayo yaweza kukuhekimisha hata upate wokovu kwa imani iliyo katika Kristo Yesu.”

 

2Timotheo 1:5-7 “Nami natamani sana kukuona, nikiyakumbuka machozi yako, ili nijae furaha; nikiikumbuka imani uliyo nayo isiyo na unafiki, ambayo ilikaa kwanza katika bibi yako Loisi, na katika mama yako Eunike, nami nasadiki wewe nawe unayo. Kwa sababu hiyo nakukumbusha, uichochee karama ya Mungu, iliyo ndani yako kwa kuwekewa mikono yangu. Maana Mungu hakutupa roho ya woga, bali ya nguvu na ya upendo na ya moyo wa kiasi.”

 

Matendo 16:1-3 “Basi akafika Derbe na Listra, na hapo palikuwa na mwanafunzi mmoja jina lake Timotheo, mwana wa mwanamke Myahudi aliyeamini; lakini babaye alikuwa Myunani. Mtu huyo alishuhudiwa vema na ndugu waliokaa Listra na Ikonio.Paulo akamtaka huyo afuatane naye, akamtwaa akamtahiri kwa ajili ya Wayahudi waliokuwako pande zile; kwa maana wote walijua ya kuwa babaye ni Myunani.”

                                                       

Jinsi ya kufanikisha huduma ya watoto

Watoto ni urithi wa Mungu, kwa maana ya kwamba Mungu anataka kuwekeza kwa watoto kwa faida ya ufalme wake na kazi yake ya baadae wakati ambapo adui naye anakusudia kuwamaliza mapema ili waweze kutimiza mapenzi yake hapa duniani, kwa msingi huo kama kanisa hatuna budi kuhakikisha kuwa tunawekeza nguvu zetu mapema ili kujikinga na yale yaliyotokea wakati wa  waamuzi baada ya kifo cha Yoshua ambako kuliinuka kizazi ambacho hakikumjua Mungu wala matendo yake, Ni huduma ya watoto ndiyo itakayolinda kizazi kijacho, na bila ya hivyo tutakatikia sehemu fulani na kuishia hapo, kwa hiyo ni muhimu kwa kila kanisa na watendakazi  na wahudumu wa injili kuhakikisha tunaifanikisha huduma hii  ya watoto kwa gharama yoyote ile Lazima kila kanisa:

Kuweko na maono kwa maswala ya watoto Mithali 29:17-18 “Mrudi mwanao naye atakustarehesha; Naam, atakufurahisha nafsi yako. Pasipo maono, watu huacha kujizuia; Bali ana heri mtu yule aishikaye sheria.”

Walimu walioandaliwa vema – Huduma ya walimu wa watoto ni wito maalumu kabisa sio kila mtu anaweza kuwahudumia watoto, kwa hiyo lazima kuweko mkakati wa kuwapata na kuwaleta kwa Yesu walimu, waliookoka, wanaowapenda watoto, wenye mzigo na wenye huduma hii, hata kama wamesomea ualimu wa awali pia lakini wawe wamejazwa Roho Mtakatifu, wanaopenda watoto, wenye uvumilivu na subira wanaojua kuchukuliana nao wenye kuomba na wawe mfano wa kuigwa

Waefeso 4:11-12 “Naye alitoa wengine kuwa mitume, na wengine kuwa manabii; na wengine kuwa wainjilisti na wengine kuwa wachungaji na waalimu; kwa kusudi la kuwakamilisha watakatifu, hata kazi ya huduma itendeke, hata mwili wa Kristo ujengwe; hata na sisi sote tutakapoufikia umoja wa imani na kumfahamu sana Mwana wa Mungu, hata kuwa mtu mkamilifu, hata kufika kwenye cheo cha kimo cha utimilifu wa Kristo;”

Kuandaliwa kwa mfumo wa mafundisho yanayofaa - Watoto wana namna yao ya kufundishwa, zinaweza kutumika hadithi za kibiblia, michoro, michezo yenye ujumbe, mistari ya kukariri, uimbaji, nyimbo, na lugha inayoendana na umri wao, ikiwa kwa watu wazima kuna maziwa na chakula kigumu basi ni zaidi sana lazima kuwe na namna njema ya kuwekeza mafundisho kwa watoto wadogo kulingana na umri wao pia

Waebrania 5:11-14 “Ambaye tuna maneno mengi ya kunena katika habari zake; na ni shida kuyaeleza kwa kuwa mmekuwa wavivu wa kusikia. Kwa maana, iwapasapo kuwa waalimu, (maana wakati mwingi umepita), mnahitaji kufundishwa na mtu mafundisho ya kwanza ya maneno ya Mungu; nanyi mmekuwa mnahitaji maziwa wala si chakula kigumu. Kwa maana kila mtu atumiaye maziwa hajui sana neno la haki, kwa kuwa ni mtoto mchanga. Lakini chakula kigumu ni cha watu wazima, ambao akili zao, kwa kutumiwa, zimezoezwa kupambanua mema na mabaya.”

Mazingira salama, uadilifu na ushirikiano na wazazi - Watoto wanahitaji ulinzi na usalama wa kimwili, kiroho na kihisia, kwa msingi huo ni lazima kanisa lijiwekee kanuni za ulinzi wa Mtoto, tuwatengenee mazigira rafiki yasiyo na unyanyasaji na ushirikiano mkubwa na wazazi hatuwezi kuwapata watoto kwa sababu wako chini ya mamlaka ya wazazi wao kwa hiyo ni lazima wazazi watoe ushirikiano mkubwa ikiwa ni pamoja na kuwaleta ibadani au kuwaleta katika makusanyiko na makambi ya makongamano ya watoto, Yusufu na Mariamu hawakuacha kumpeleka Yesu Hekaluni tangu wakati wa utoto wake, mpaka ikatokea kuwa mtoto huyu akawa anapenda kujifunza neno.

Luka 2:21-24 “Hata zilipotimia siku nane za kumtahiri, aliitwa jina lake Yesu; kama alivyoitwa na malaika kabla hajachukuliwa mimba.Kisha, zilipotimia siku za kutakasika kwao, kama ilivyo torati ya Musa walikwenda naye hata Yerusalemu, wamweke kwa Bwana,(kama ilivyoandikwa katika sheria ya Bwana, Kila mtoto mwanamume aliye kifungua mimba ya mamaye na aitwe mtakatifu kwa Bwana),wakatoe na sadaka, kama ilivyonenwa katika sheria ya Bwana, Hua wawili au makinda ya njiwa wawili

Luka 2:40-46 “Yule mtoto akakua, akaongezeka nguvu, amejaa hekima, na neema ya Mungu ilikuwa juu yake. Basi, wazee wake huenda Yerusalemu kila mwaka, wakati wa sikukuu ya Pasaka. Na alipopata umri wake miaka kumi na miwili, walipanda kama ilivyokuwa desturi ya sikukuu; na walipokwisha kuzitimiza siku, wakati wa kurudi kwao, yule mtoto Yesu alibaki nyuma huko Yerusalemu, na wazee wake walikuwa hawana habari. Nao wakadhani ya kuwa yumo katika msafara; wakaenenda mwendo wa kutwa, wakawa wakimtafuta katika jamaa zao na wenzao; na walipomkosa, wakarejea Yerusalemu, huku wakimtafuta. Ikawa baada ya siku tatu wakamwona hekaluni, ameketi katikati ya waalimu, akiwasikiliza na kuwauliza maswali.”

Mwisho kabisa maombi ni jambo la msingi sana kwa huduma hii, kama tunavyojua kila kitu cha kiroho kinahitaji maombi basi ni muhimu kwetu kuhakikisha kuwa kama kutakuwa na huduma hii basi walimu wake waombewe, na watoto waombewe na wazazi waombewe na kwa ujumla watoto waombewe na wafunguliwe vilevile kama tunavyowasikiliza watu wazima na kuwaombea

Rev. Innocent Samuel Kamote

Mkuu wa wajenzi mwenye Hekima

Jumatano, 26 Agosti 2026

Nafasi ya Mwanaume Katika huduma!


1Timotheo 2:5-8 “Kwa sababu Mungu ni mmoja, na mpatanishi kati ya Mungu na wanadamu ni mmoja, Mwanadamu Kristo Yesu; ambaye alijitoa mwenyewe kuwa ukombozi kwa ajili ya wote, utakaoshuhudiwa kwa majira yake. Nami kwa ajili ya huo naliwekwa niwe mhubiri na mtume, (nasema kweli, sisemi uongo), mwalimu wa Mataifa katika imani na kweli. Basi, nataka wanaume wasalishe kila mahali, huku wakiinua mikono iliyotakata pasipo hasira wala majadiliano.”




Utangulizi:

Ni muhimu kufahamu kuwa wanaume ni mojawapo ya nguzo muhimu sana katika jamii na katika Kanisa pia, Kanisa lolote ambalo lina afya ya kiroho kamwe haliwezi kupuuzia ujenzi wa wanaume kama wanafunzi wa Yesu ambao wanawajibika kwa kiwango kikubwa katika usimamizi wa jamii, familia na Kanisa, Kanisa linapoweka mkakati kuwaelimisha vizuri wanaume ni dhahiri litapata nguzo muhimu za kiroho zenye nguvu, ushawishi na mamlaka ya kuibadili jamii na kuileta kwa Kristo.

Marko 3:13-19 “Akapanda mlimani, akawaita aliowataka mwenyewe; wakamwendea.  Akaweka watu kumi na wawili, wapate kuwa pamoja naye, na kwamba awatume kuhubiri, tena wawe na amri ya kutoa pepo. Akawaweka wale Thenashara; na Simoni akampa jina la Petro; na Yakobo, mwana wa Zebedayo, na Yohana nduguye Yakobo, akawapa jina la Boanerge, maana yake, wana wa ngurumo; na Andrea, na Filipo, na Bartholomayo, na Mathayo, na Tomaso, na Yakobo wa Alfayo, na Thadayo, na Simoni Mkananayo, na Yuda Iskariote, ndiye aliyemsaliti. Kisha akaingia nyumbani.”

Kutokana na umuhimu wa wanaume Yesu kwanza aliwaita wanaume 12 ili wawe  pamoja naye  na wawe wanafunzi wake wa msingi, kwa kusudi la kuwafundisha ili kisha waweze kubeba jukumu la kuweka msingi wa kanisa kwa kujenga utamaduni mpya jamii mpya na taifa jipya yaani Kanisa la Mungu ambao ni kama Israel ya Kiroho, Yesu alitamani wajifunze maisha yake ya kila siku, tabia zake na mafundisho yake, kisha wasambaze ujumbe wake wa ufalme wa Mungu, huku wakiwa na mamlaka ya kuponya wagonjwa na kutoa pepo, Yesu hakupuuza wanawake lakini alionyesha wazi kuwa wanaume wana umuhimu mkubwa zaidi katika maongozi ya Kanisa kama ilivyokuwa wana wa Israel 12 ambao walikuwa kabila 12 za Israel ambazo zilikuwa chanzo cha taifa la Israel, kwa sababu hiyo Yesu hata leo bado anawategemea sana wanaume katika kazi yake. Kwa msingi huo leo tutachukua muda kujifunza somo hili muhimu Nafasi ya Mwanaume katika huduma kwa kuzingatia vipengele muhimu vikuu vitatu vifuatavyo:-

·         Umuhimu wa mwanaume kwa mujibu wa maandiko

·         Wajibu wa mwanaume kwa mujibu wa maandiko

·         Nafsi ya Mwanaume katika huduma

Umuhimu wa mwanaume kwa mujibu wa maandiko.

Ni muhimu kufahamu kuwa mwanaume ana wajibu mkubwa na wa kwanza kabisa katika jamii duniani kama ilivyo vile vile katika Kanisa mwanaume amaeaminiwa uwakili na Mungu, Mwanaume ni mfadhili, mwamaume ni mlinzi, mwanaume ni mpiganaji, mwanaume ni kiongozi, wakati Mungu anaiumba dunia katika mpango wake mwanaume alipewa kipaumbele kama kiumbe wa kwanza anayeweza kuendeleza na kutunza uumbaji wa Mungu duniani, kule kuumbwa kwanza kulimfanya awe kiongozi wa asili

Mwanzo 2:15-17 “BWANA Mungu akamtwaa huyo mtu, akamweka katika bustani ya Edeni, ailime na kuitunza. BWANA Mungu akamwagiza huyo mtu, akisema, Matunda ya kila mti wa bustani waweza kula, walakini matunda ya mti wa ujuzi wa mema na mabaya usile, kwa maana siku utakapokula matunda ya mti huo utakufa hakika.”

1Timotheo 2:11-15 “Mwanamke na ajifunze katika utulivu, akitii kwa kila namna.Simpi mwanamke ruhusa ya kufundisha, wala kumtawala mwanamume, bali awe katika utulivu.Kwa maana Adamu ndiye aliyeumbwa kwanza, na Hawa baadaye. Wala Adamu hakudanganywa, ila mwanamke alidanganywa kabisa akaingia katika hali ya kukosa.Walakini ataokolewa kwa uzazi wake, kama wakidumu katika imani na upendo na utakaso, pamoja na moyo wa kiasi.

Maandiko yanaonyesha kuwa mwanaume ni nguzo muhimu sana katika jamii na  imani na kuwa anamchango mkubwa sana katika maswala ya ujenzi wa jamii kuanzia na maswala ya kiroho, uongiozi wa familia, ujenzi wa jamii, uchumi, kufanya kazi, na kuwafundisha wengine, Jamii yoyote yenye afya ya kijamii ni ile ambayo wanaume wako mstari wa mbele katika kila jambo, kwa hiyo wanaume wakitangulia huku wakisaidiwa na wanawake wanauwezo mkubwa sana ya kuifanya jamii hiyo kuwa na nguvu likiwepo Kanisa, Kwa bahati mbaya tuko katika nyakati ambazo sasa ambao uanaume unapigwa vita sana au wanaume wanaacha wajibu wao na kuanza kutaka vya dezo, kufanyiwa na kuandalia kila kitu jambo ambalo litatujengea jamii ya ajabu sana na Kanisa la ajabu pia, Mungu alimchagua mwanaume mmoja jina lake Abrahamu kwa sababu alimjua kuwa mwanaume huyu atakuwa mjenzi wa jamii yake hata baada yake akiwafundisha watoto wake baada yake washike hukumu za Mungu na kutenda haki

Mwanzo 15:17-19 “BWANA akanena, Je! Nimfiche Ibrahimu jambo nilifanyalo, akiwa Ibrahimu atakuwa taifa kuu, hodari, na katika yeye mataifa yote ya dunia watabarikiwa? Kwa maana nimemjua ya kwamba atawaamuru wanawe, na nyumba yake baada yake waishike njia ya BWANA, wafanye haki na hukumu, ili kwamba BWANA naye akamtimizie Ibrahimu ahadi zake.”

Maandiko yanaonyesha kuwa wanaume wana umuhimu mkubwa sana katika ujenzi wa jamii inayomcha Mungu, jamii inayofanyakazi, jamii yenye ugunduzi, jamii yenye maendeleo, yenye utulivu na mwelekeo mkubwa wa maendeleo ya kiroho, kimwili, kisayansi na kisaikolojia, bila kujali sera kubwa za sasa zinazokazania usawa wa kijinsia na utambuzi wa wanawake katika jamii, lakini hii haiondoi ukweli wa neno la Mungu kuwa wanaume wana mchango wakipekee kuanzia katika usimamizi wa kifamilia  mapaka katika maswala ya ibada, uchumi na ugunduzi wa teknolojia. Wanaume bado wanabaki kuwa ndio washikadau wakubwa wa mwelekeo wa ulimwengu na kwakweli Mungu anawategemea sana wanaume na anataka wawe mstari wa mbele kila mahali

Kama unadhani wanaume sio wa muhimu fanya utafiti mdogo tu waulizie wanawake ambao wameishi kama “Single Mothers” kwa muda flani utagundua tu kuwa wana changamoto kubwa zaidi na mateso makubwa ya kihisia wakiteswa na upweke, kiburi, migandamizo na mateso ya kihisia wengi wanalia na hata wakikutana na mambo magumu wanasema ninaonewa kwa sababu sina Mume, Mungu alimuumba kila mwanadamu na upekee wake na kila mmoja anamtegemea mwingine kwa hiyo haijalishi mwanamke atakuwa na mafanikio makubwa kiasi gani  lakini utafiti unaonyesha kuwa bila mwanaume mwanamke huyo hana ukamilifu. Mungu ameumba watoto wakue wakisikia sauti ya baba na mama na wanapoikosa sauti mojawapo watakapokuwa watu wazima wataanza kuuliza yuko wapi baba yangu? au wataonyesha athari zinazoashiria kukosekana kwa malezi ya upande mmoja

Na ndio maana leo neno la Mungu linawataka wanaume wasimame katika nafasi yao kuanzia katika ibada mpaka katika majukumu mengine ya kijamii, kama hesabu za Agano la kale zingekuwa zinafanya kazi hata leo, Kanisa letu unadhani lingekuwa na washirika wangapi?  Ninene kiwazimu kila mchungaji asihesabu washirika wanawake, ahesabie wanaume tu kisha tuone!

Mathayo 14:19-21. “Akawaagiza makutano waketi katika majani; akaitwaa ile mikate mitano na wale samaki wawili, akatazama juu mbinguni, akabariki, akaimega ile mikate, akawapa wanafunzi, wanafunzi wakawapa makutano.Wakala wote wakashiba; wakayaokota masazo ya vipande vya mikate, vikapu kumi na viwili, vimejaa. NAO WALIOKULA WALIKUWA WANAUME WAPATA ELFU TANO, bila wanawake na watoto.”             

Muulize jirani yako hapo Mtumishi hiyo miujiza unayoifanya unawafanyia wanaume wangapi? Yesu alifanya miujiza mbele ya wanaume 5000 bila kuhesabu wanawake na watoto, Muulize tena miujiza yako inafanyika mbele ya nani? muulize Kanisa lako wewe ulianza na kina nani? Tunasoma kuwa Kanisa la Efeso lilianza na wanaume 12 tu na walipompokea Roho Mtakatifu kazi ya Mungu ilienea na Kanisa lilikuwa kubwa sana, nadhani kama tungekuwa tunahesabia wanaume tu kanisani basi utagundua kuwa bado makanisa mengi yanalazimika kuwa na wajibu wa kuwafikia wanaume na tukiwa na wanaume wengi tuna washirika wengi

Matendo 19:1-7 “Ikawa, Apolo alipokuwa Korintho, Paulo, akiisha kupita kati ya nchi za juu, akafika Efeso; akakutana na wanafunzi kadha wa kadha huko; akawauliza, Je! Mlipokea Roho Mtakatifu mlipoamini? Wakamjibu, La, hata kusikia kwamba kuna Roho Mtakatifu hatukusikia. Akawauliza, Basi mlibatizwa kwa ubatizo gani? Wakasema, Kwa ubatizo wa Yohana.Paulo akasema, Yohana alibatiza kwa ubatizo wa toba, akiwaambia watu wamwamini yeye atakayekuja nyuma yake, yaani, Yesu. Waliposikia haya wakabatizwa kwa jina la Bwana Yesu.Na Paulo, alipokwisha kuweka mikono yake juu yao, Roho Mtakatifu akaja juu yao; wakaanza kunena kwa lugha, na kutabiri.Na jumla yao walipata wanaume kumi na wawili.”

Paulo mtume anamwambia Timotheo nataka wanaume wasimame kila mahali, hili lilikuwa ni agizo la Mungu kwa Kanisa hata leo, Mungu anawataka wanaume, katika mikakati yetu ya kuihubiri injili ni muhimu kwetu tukae tujadili na kutafakari kwamba tunajali ni kwa namna gani tutawapata wanaume? wanaume wakipataikana na wakawa wanasali na kuinua mikono iliyotakata jamii nzima itabadilika, Shetani amewachukua wanaume kwenye mpira wa soka, amewachukua baa na kanisani anatuachia wanawake na kanisa tumekaa na kutumbua macho, mwambie jirani yako nataka wanaume hapa, Basi nataka wanaume wasalishe kila mahali!

1Timotheo 2:8 “Basi, nataka wanaume wasalishe kila mahali, huku wakiinua mikono iliyotakata pasipo hasira wala majadiliano.”

Wajibu wa mwanaume kwa mujibu wa maandiko.

Kufanya kazi kwa mikono yake mwenyewe – Moja ya wajibu aliopewa mwanaume hapa duniani ni kufanya kazi, Kazi ina Baraka nyingi sana hata kama mtu hajaokoka akifanya kazi kazi huleta matokeo makubwa, Nchi nyingi zenye mafanikio na maendeleo makubwa ni nchi za watu wanaofanya kazi na sio wale wanaopiga soga, Kazi ilikuwa ni wajibu wa kwanza aliopewa mwanadamu hata kabla ya kuagizwa kuabudu, Mungu aliagiza wanadamu wafanye kazi, Mungu mwenyewe aliumba dunia kwa kufanya kazi siku sita, kwa hiyo ni lazima tufanye kazi, maandiko yanaagiza kila mwanaume kufanya kazi, kazi ni wajibu ni ibada.

Mwanzo 2:15-17 “BWANA Mungu akamtwaa huyo mtu, akamweka katika bustani ya Edeni, ailime na kuitunza. BWANA Mungu akamwagiza huyo mtu, akisema, Matunda ya kila mti wa bustani waweza kula, walakini matunda ya mti wa ujuzi wa mema na mabaya usile, kwa maana siku utakapokula matunda ya mti huo utakufa hakika.”

2Wathesalonike 3:6-10 “Ndugu, twawaagiza katika jina la Bwana Yesu Kristo, jitengeni nafsi zenu na kila ndugu aendaye bila utaratibu, wala si kwa kufuata mapokeo mliyoyapokea kwetu. Mwajua wenyewe jinsi iwapasavyo kutufuata; kwa sababu hatukuenda bila utaratibu kwenu; wala hatukula chakula kwa mtu ye yote bure; bali kwa taabu na masumbufu, usiku na mchana tulitenda kazi, ili tusimlemee mtu wa kwenu awaye yote. Si kwamba hatuna amri, lakini makusudi tufanye nafsi zetu kuwa kielelezo kwenu, mtufuate. Kwa kuwa hata wakati ule tulipokuwapo kwenu tuliwaagiza neno hili, kwamba ikiwa mtu hataki kufanya kazi, basi, asile chakula.”                

Mwanaume anapaswa kuwa na Ushujaa, - Maisha ya duniani ni kama mapambano na njia mojawapo ya kufanikiwa ni pamoja na kuwa na ushujaa, kujiamini kuwa mbali na woga na hofu, kila mwanaume anapaswa kumcha Mungu na kumtegemea Mungu lakini kujiamini na kujipa ujasiri, hakuna mafanikio kama hutakuwa na ujasiri, odoa aibu jipe ujasiri pambania hatima ya jamii yako

Yoshua 1:7-9 “Uwe hodari tu na ushujaa mwingi, uangalie kutenda sawasawa na sheria yote aliyokuamuru Musa mtumishi wangu; usiiache, kwenda mkono wa kuume, au wa kushoto, upate kufanikiwa sana kila uendako. Kitabu hiki cha torati kisiondoke kinywani mwako, bali yatafakari maneno yake mchana na usiku, upate kuangalia kutenda sawasawa na maneno yote yaliyoandikwa humo; maana ndipo utakapoifanikisha njia yako, kisha ndipo utakapositawi sana. Je! Si mimi niliyekuamuru? Uwe hodari na moyo wa ushujaa; usiogope wala usifadhaike; kwa kuwa Bwana, Mungu wako, yu pamoja nawe kila uendako.”

1Wafalme 2:1-4 “Basi siku ya kufa kwake Daudi ikakaribia, akamwusia Sulemani mwanawe, akasema, Mimi naenda njia ya ulimwengu wote; basi uwe hodari, ujionyeshe kuwa mwanamume; uyashike mausia ya Bwana, Mungu wako, uende katika njia zake, uzishike sheria zake, na amri zake, na hukumu zake, na shuhuda zake, sawasawa na ilivyoandikwa katika torati ya Musa, upate kufanikiwa katika kila ufanyalo, na kila utazamako, ili Bwana afanye imara neno lake alilonena kwa habari yangu, akisema, Ikiwa watoto wako wataiangalia njia yao, wakienda mbele zangu kwa kweli, kwa moyo wao wote, na kwa roho yao yote, (akasema), hutakosa mtu katika kiti cha enzi cha Israeli.”

1Wakorintho 16:13-14 “Kesheni, simameni imara katika Imani, fanyeni kiume, mkawe hodari. Mambo yenu yote na yatendeke katika upendo.”

Wanaume wanaagizwa kumpenda Mungu – Kila mwanaume anawajibu wa kumpenda Mungu, Mwanaume aliwekwa duniani na Mungu kabla ya wanawake na mambo mengine, Mungu alimchagua mwanaume kuwa mtumishi wake, alikuwa amekusudia awe na uhusiano na yeye, furaha ya mwanaume mkamilifu kamwe haiwezi kuwa kamili kama hana uhusiano mwema na Mungu, Maandiko yanaamuru tumpende Bwana Mungu wetu kwa moyo, kwa akili na kwa nguvu na jirani zetu kama nafsi zetu.

Mathayo 22:37-39 “Akamwambia, Mpende Bwana Mungu wako kwa moyo wako wote, na kwa roho yako yote, na kwa akili zako zote. Hii ndiyo amri iliyo kuu, tena ni ya kwanza.Na ya pili yafanana nayo, nayo ni hii, Mpende jirani yako kama nafsi yako.”

Wanaume waagiza kuwa na familia – Mojawapo ya wajibu muhumu wa kila mwanaume ni kuanzisha familia kwa hiyo mwanaume ni kiongozi kipenzi wa mkewe, kila mwanaume anatakiwa kuanzisha na kusimamia familia yenye mamlaka na familia imara akiwa msimamizi wa imani, tamaduni, sheria na taratibu za kiungu katika familia hiyo, familia itakayostawisha na mwanaume haiwezi kuwa imara kama mwanaume huyo atamweka Kristo pembeni, mamlaka ya mwanaume inaweza kuwa kamili na ya amani kama itifaki ya kiungu itakaa sawa katika familia hiyo na mwanaume anawajibika kuipenda familia yake na kuisimamia na kuilinda na kuhakikisha kuwa anaipatia mahitaji yao, wale wanaoogopa majukumu na wanaoogopa kuoa na kuwa na familia uanaume wao hauwezi kuwa uanaume kamili, Mwanaume hapaswi kuogopa majukumu wala hapaswi kuyakimbia, wengi leo wamekimbia familia

1Wakorintho 11:3 “Lakini nataka mjue ya kuwa kichwa cha kila mwanamume ni Kristo, na kichwa cha mwanamke ni mwanamume, na kichwa cha Kristo ni Mungu.”

Waefeso 5:25-29 “Enyi waume, wapendeni wake zenu, kama Kristo naye alivyolipenda Kanisa, akajitoa kwa ajili yake;  ili makusudi alitakase na kulisafisha kwa maji katika neno; apate kujiletea Kanisa tukufu, lisilo na ila wala kunyanzi wala lo lote kama hayo; bali liwe takatifu lisilo na mawaa. Vivyo hivyo imewapasa waume nao kuwapenda wake zao kama miili yao wenyewe. Ampendaye mkewe hujipenda mwenyewe. Maana hakuna mtu anayeuchukia mwili wake po pote; bali huulisha na kuutunza, kama Kristo naye anavyolitendea Kanisa.”

Wanaume wanawajibika kutawala au kuongoza – Itifaki ya kiutawala na kiuongozi katika familia  inaonyesha kuwa mwanaume ndiye anatakiwa kuwa Kichwa, neno kichwa  ambalo kwenye kiingereza limetajwa kama  the head” katika lugha ya Kiyunani ni  “KephalÄ“ ambalo maana yake ni the brain  literal na Metaphorical ni Chief, Ruler, Leader, Master, au  a person of high status au the source kwa hiyo kama Kristo alivyo ndiye mkuu wa Kanisa na mume ndiye mkuu wa familia na mkuu wa mke wake utaratibu huu ukikiukwa hata kama hamjafanya dhambi uwepo wa Mungu unaondoka Mungu ni Mungu wa utaratibu na sio Mungu wa machafuko, kwa hiyo mume anawajibu wa kuongoza na kutawala katika ndoa yake “be the head of your wife” hili ni agizo:-  

Mwanzo 3:16-19 “Akamwambia mwanamke, Hakika nitakuzidishia uchungu wako, na kuzaa kwako; kwa utungu utazaa watoto; na tamaa yako itakuwa kwa mumeo, naye atakutawala. Akamwambia Adamu, Kwa kuwa umeisikiliza sauti ya mke wako, ukala matunda ya mti ambao nalikuagiza, nikisema, Usiyale; ardhi imelaaniwa kwa ajili yako; kwa uchungu utakula mazao yake siku zote za maisha yako; michongoma na miiba itakuzalia, nawe utakula mboga za kondeni; kwa jasho la uso wako utakula chakula, hata utakapoirudia ardhi, ambayo katika hiyo ulitwaliwa; kwa maana u mavumbi wewe, nawe mavumbini utarudi.”

Waefeso 5:23-26 “Kwa maana mume ni kichwa cha mkewe, kama Kristo naye ni kichwa cha Kanisa; naye ni mwokozi wa mwili. Lakini kama vile Kanisa limtiivyo Kristo vivyo hivyo wake nao wawatii waume zao katika kila jambo.Enyi waume, wapendeni wake zenu, kama Kristo naye alivyolipenda Kanisa, akajitoa kwa ajili yake; ili makusudi alitakase na kulisafisha kwa maji katika neno;”                

Wanaume wanawajibu wa kusalisha – Kama jinsi ambavyo wanaume wamepewa wajibu wa kuwa viongozi wa familia, Mungu amewapa wajibu pia wa kusimamia shughuli za ibada kila mahali, Mungu anawapa wajibu sio tu kusimamia ibada lakini kuwa kielelezo kikubwa cha imani katika familia yake, Neno kusalisha katika Kiyunani ni “Proseuchomai” limetumika mara 90 katika agano jipya kwa kiingereza “to supplicate worship”, au “to be a person in authority to God during prayer” Paulo anawataka wanaume huko Efeso wawe viongozi wa ibada kila mahali, waongoze maombi, waongoze ibada wasalishe

1Timotheo 2:5-8 “Kwa sababu Mungu ni mmoja, na mpatanishi kati ya Mungu na wanadamu ni mmoja, Mwanadamu Kristo Yesu; ambaye alijitoa mwenyewe kuwa ukombozi kwa ajili ya wote, utakaoshuhudiwa kwa majira yake. Nami kwa ajili ya huo naliwekwa niwe mhubiri na mtume, (nasema kweli, sisemi uongo), mwalimu wa Mataifa katika imani na kweli. Basi, nataka wanaume wasalishe kila mahali, huku wakiinua mikono iliyotakata pasipo hasira wala majadiliano.”

Nafasi ya Mwanaume katika huduma!

1Timotheo 2:5-8 “Kwa sababu Mungu ni mmoja, na mpatanishi kati ya Mungu na wanadamu ni mmoja, Mwanadamu Kristo Yesu; ambaye alijitoa mwenyewe kuwa ukombozi kwa ajili ya wote, utakaoshuhudiwa kwa majira yake. Nami kwa ajili ya huo naliwekwa niwe mhubiri na mtume, (nasema kweli, sisemi uongo), mwalimu wa Mataifa katika imani na kweli. Basi, nataka wanaume wasalishe kila mahali, huku wakiinua mikono iliyotakata pasipo hasira wala majadiliano.”

Pauilo mtume hataki wanaume wabweteke tu kanisani anatoa wito kwa kila kanisa kuwa wanaume ndio wawe mstari wa mbele katika kila mkutaniko wa Kanisa la Mungu tena sio waje tu mbele na kuongoza ibada kila mahali lakini pia wakiwa na mikono safi, maana yake wakiwa na maisha matakatifu, wanaume wawe kielelezo, kuwa na mikono iliyotakata maana yake ni wasio na hatia, walio safi kimaadili, Yesu Kristo mwokozi wetu alikuwa mwanaume, ukombozi wetu umetoka kwa mwanaume kwa hiyo kila mwanaume anatakiwa kuwa mstari wa mbele katika kumuunga mkono mwokozi wetu na sio kukaa nyuma nyuma

Isaya 9:6-7 “Maana kwa ajili yetu mtoto amezaliwa, Tumepewa mtoto mwanamume; Na uweza wa kifalme utakuwa begani mwake; Naye ataitwa Jina Lake, Mshauri wa ajabu, Mungu mwenye nguvu, Baba wa milele, Mfalme wa amani. Maongeo ya enzi yake na amani Hayatakuwa na mwisho kamwe, Katika kiti cha enzi cha Daudi na ufalme wake; Kuuthibitisha na kuutegemeza Kwa hukumu na kwa haki, Tangu sasa na hata milele. Wivu wa Bwana wa majeshi ndio utakaotenda hayo.”

Paulo kwa kusema agizo lake lile alikuwa anamtaka Timotheo kuhakikisha anawekeza kwa wanaume maswala ya kiroho yote kama mwanaume ndio kiongozi wa familia kumchukua mke wake na watoto wake kuja ibadani kisha kumuacha yeye ni sawa na kuteka ufalme wake, na utawala wake.  Kanisa lazima limlenge mwanaume hata kama mwanamke ataokoka kwanza lakini lazima zitafutwe namna na baba afuate nyakati za kanisa la kwanza alikuwa akiokoka baba kwanza na nyumba nzima inafuata, na sio hivyo tu Mwanaume akitangaza msimamo moja kwa moja na familia nzima iliweza kuhusika kuliko mwanamke akitangaza.  

Matendo 10:1-5 “Palikuwa na mtu Kaisaria, jina lake Kornelio, akida wa kikosi kilichoitwa Kiitalia, mtu mtauwa, mchaji wa Mungu, yeye na nyumba yake yote, naye alikuwa akiwapa watu sadaka nyingi, na kumwomba Mungu daima. Akaona katika maono waziwazi, kama saa tisa ya mchana, malaika wa Mungu, akimjia na kumwambia, Kornelio! Akamtazama sana, akaogopa akasema, Kuna nini, Bwana? Akamwambia, Sala zako na sadaka zako zimefika juu na kuwa ukumbusho mbele za Mungu. Sasa basi, peleka watu Yafa, ukamwite Simoni, aitwaye Petro.”

Matendo 16:27-32 “Yule mlinzi wa gereza akaamka, naye alipoona ya kuwa milango ya gereza imefunguka, alifuta upanga, akataka kujiua, akidhani ya kuwa wafungwa wamekimbia. Ila Paulo akapaza sauti yake kwa nguvu, akisema, Usijidhuru, kwa maana sisi sote tupo hapa. Akataka taa ziletwe, akarukia ndani, akitetemeka kwa hofu, akawaangukia Paulo na Sila; kisha akawaleta nje akasema, Bwana zangu, yanipasa nifanye nini nipate kuokoka? Wakamwambia, Mwamini Bwana Yesu, nawe utaokoka pamoja na nyumba yako.Wakamwambia neno la Bwana, yeye na watu wote waliomo nyumbani mwake.”

Yoshua 24:14-16. “Basi sasa mcheni Bwana, mkamtumikie kwa unyofu wa moyo na kwa kweli; na kuiweka mbali miungu ambayo baba zenu waliitumikia ng'ambo ya Mto, na huko Misri; mkamtumikie yeye Bwana. Nanyi kama mkiona ni vibaya kumtumikia Bwana, chagueni hivi leo mtakayemtumikia; kwamba ni miungu ile ambayo baba zenu waliitumikia ng'ambo ya Mto, au kwamba ni miungu ya wale Waamori ambao mnakaa katika nchi yao; lakini mimi na nyumba yangu tutamtumikia Bwana. Hao watu wakajibu wakasema, Hasha! Tusimwache Bwana, ili kuitumikia miungu mingine;”            

Mungu akianza na wanaume katika kuokoa ni ukweli ulio wazi kuwa wanawake watafuata tu na watoto pia na migogoro mingi ya watu kuachwa kwaajili ya wokovu itakuwa haiko, hivi ndio Mungu anavyotaka, wanaume wakiwa mstari wa mbele katika mikesha kutakuwa na mafarakano nyumbani kweli? Mwanaume akitangaza msimamo wengine watafuata tu Basi, nataka wanaume wasalishe kila mahali, Mungu anatamani wanaume wawe kama Yoshua watangaze msimamo na familia zao zifuate

1.     Kanisa tusiwasahauu wanaume - Kanisa lolote lenye afya njema na familia yoyote yenye afya njema itampa mwanaume kipaumbele, tunapoweka mipango yetu na maombi yetu kwaajili ya wanaume ili waokolewe hata kama hawatakuwa viongozi kanisani watakuwa viongozi katika familia zao na jamii, wanaume wana nafasi kubwa ya kuvunja kuta zote za vizuizi katika jamii na familia na kuwa sauti ya Yesu Kristo kila mahali, mwanaume akipatikana jamii nzima itapatikana  na ndio maana Paulo anataka wanaume wasalishe kila mahali, Yesu mwenye nguvu ya kuokoa hataokoa kwa uonevu ataiokoa wanaume pia

 

1Wakorintho 16:13-14. “Kesheni, simameni imara katika Imani, fanyeni kiume, mkawe hodari. Mambo yenu yote na yatendeke katika upendo.”

 

2.  Kanisa lazima liwaendeleze wanaume kama viongozi wa kiroho, Yesu hakuufikia ulimwengu kwa kuzungumza na watu wengi pee yake lakini aliwekeza muda mwingi, mrefu na wakutosha akiwa na wanaume 12 aliwaandaa kuwa viongozi, aliwatia moyo na kuwajenga ili kuwekeza ukomavu wa kiroho kwao, hebu fikiria nyumba ambayo mama amekomaa kiroho afu baba ni mchanga kiroho?  Ukomavu wa kiroho ukiwekezwa kwa wanaume tunatengeneza jamii yenye amani sawasawa na mpango wa Mungu, ukuaji wa kiroho ni swala linalohiaji mpango, na wanaume kwa taarifa yako ndio wenye ushawishi mkubwa utafiti wa kweli unaonyesha kuwa mama akitangulia kuokoka ni asilimia 30% ya wanafamilia ndio watakaomfuata lakini baba akitangulia kuokoka ni asilimia 93% ya wanafamilia watafuta kwa hiyo tunapopanga kuufikia ulimwengi fikiria namna ya kuwapata wanaume, mafunzo na mafundisho ya kimkakati kanisani yasikose kufikiri kuwafikia wanaume.

 

3.    Kanisa linalotaka kukua ni lazima lilenge kuwahudumia au kuwafikia wanaume – Mungu hajawapuuzia wanaume agizo la Paulo kwa Timotheo linasisitiza kwamba wanaume wahudumiwe kwa wingi na kwa kadiri iwezekanavyo, tutengeneze Ujamaa na wanaume kama neno la Mungu lisemavyo kuwa chuma hunoa chuma, tuwanoe Wanaume tuwafikie wanaume

 

Mithali 27:17-19 “Chuma hunoa chuma; Ndivyo mtu aunoavyo uso wa rafiki yake. Yeye autunzaye mtini atakula matunda yake; Naye amhudumiaye bwana wake ataheshimiwa. Kama uso ufananavyo na uso katika maji; Kadhalika moyo wa mtu na mwenzake.”

 

4.     Kila mwanaume kanisani atafute rafiki atakayesimama naye bega kwa bega kwa bega katika vita hii ya maisha, na kukumbuka ya kuwa mtu akiwa peke yake nguvu yake inakuwa ndogo lakini unapoungana na mwingine ushindi unakuwa mkubwa lakini watu wanapokuwa zaidi ya mmoja ushindi unakuwa mkubwa zaidi na hakuna atakayeweza kuwazuia maandiko yanaonyesha nguvu hizo, kimwili na kiroho

Kumbukumbu 32:29-30 “Laiti wangekuwa na akili, hata wakafahamu haya, Ili watafakari mwisho wao.Mmoja angefukuzaje watu elfu, Wawili wangekimbizaje elfu kumi, Kama Mwamba wao asingaliwauza, Kama Bwana asingaliwatoa?

Yoshua 23:9-11. “Maana Bwana amefukuza mbele yenu mataifa walio hodari, kisha wenye nguvu, lakini kwenu ninyi hapana mtu aliyesimama mbele yenu hata leo. Mtu mmoja miongoni mwenu atafukuza watu elfu; maana Bwana, Mungu wenu, ndiye anayewapigania, kama alivyowaambia. Jihadharini nafsi zenu, basi, ili mmpende Bwana, Mungu wenu.”

Mathayo 18:18-20 “ Amin, nawaambieni, yo yote mtakayoyafunga duniani yatakuwa yamefungwa mbinguni; na yo yote mtakayoyafungua duniani yatakuwa yamefunguliwa mbinguni. Tena nawaambia, ya kwamba wawili wenu watakapopatana duniani katika jambo lo lote watakaloliomba, watafanyiwa na Baba yangu aliye mbinguni. Kwa kuwa walipo wawili watatu wamekusanyika kwa jina langu, nami nipo papo hapo katikati yao.”          

Wanaume wakiigundua siri hii na kuungana na wengine kutakuwa na nguvu kubwa sana katika ufalme wa Mungu ambayo haitazuilika Mwanaume mwenye nguvu akiunga ana mwenye nguvu mwingine katika huduma unadhani kanisa litakuwa na nguvu kwa kiasi gani?  Ni kwaajili ya swala kama hili Paulo anataka wanaume wasalishe yaani washiriki maswala yote ya ibada kila mahali na maswala yote ya kiimani, na wawe mstari wa mbele katika Kanisa wakiitetea imani na kuitangaza.

5.     Kuwawezesha wanaume kutazalisha ibada zenye nguvu - Kanisa likiwapa wanaume kipaumbele kutakuwa na mafanikio makubwa sana katika kazi zake na katika maswala ya uchumi, Mwanafunzi mwanaume anapojifunza kumtumikia Mungu atamtumikia Mungu pamoja na mali zake, wanaume watataka kuona kazi ya Mungu inasonga mbele, tukiwaimarisha wanaume tutakuwa na Kanisa imara sana, tutajenga ushirika wenye kusudi, kadiri mtu anavyokua katika Kristo na kukomaa nguvu hiyo itawekezwa kwenye kanisa lake, wanaume wanaweza kutoka na kuhubiri sehemu mbalimbali, wanaweza kufanya mashambulizi yenye nguvu dhidi ya ufalme wa giza, Kanisa litakuwa lenye afya ya kiroho na ya kudumu wanaume wana nafasi kubwa zaidi na nzuri zaidi ya kutekeleza agizo kuu kuliko wanawake hata kimaumbile, fikiria Petro na Yohana!

 

Mathayo 28:18-20 “Yesu akaja kwao, akasema nao, akawaambia, Nimepewa mamlaka yote mbinguni na duniani. Basi, enendeni, mkawafanye mataifa yote kuwa wanafunzi, mkiwabatiza kwa jina la Baba, na Mwana, na Roho Mtakatifu; na kuwafundisha kuyashika yote niliyowaamuru ninyi; na tazama, mimi nipo pamoja nanyi siku zote, hata ukamilifu wa Dahari

 

Matendo 4:5-13 “Hata asubuhi wakubwa na wazee na waandishi wakakusanyika Yerusalemu, na Anasi Kuhani Mkuu, na Kayafa pia, na Yohana na Iskanda, na wote wale waliokuwa jamaa zake Kuhani Mkuu. Walipowaweka katikati wakawauliza, Kwa nguvu gani na kwa jina la nani ninyi mmefanya haya? Ndipo Petro, akijaa Roho Mtakatifu, akawaambia, Enyi wakubwa wa watu na wazee wa Israeli, kama tukiulizwa leo habari ya jambo jema alilofanyiwa yule mtu dhaifu, jinsi alivyoponywa, jueni ninyi nyote na watu wote wa Israeli ya kuwa kwa jina la Yesu Kristo wa Nazareti, ambaye ninyi mlimsulibisha, na Mungu akamfufua katika wafu, kwa jina hilo mtu huyu anasimama ali mzima mbele yenu. Yeye ndiye jiwe lile lililodharauliwa na ninyi waashi, nalo limewekwa kuwa jiwe kuu la pembeni. Wala hakuna wokovu katika mwingine awaye yote, kwa maana hapana jina jingine chini ya mbingu walilopewa wanadamu litupasalo sisi kuokolewa kwalo. Basi walipoona ujasiri wa Petro na Yohana, na kuwajua ya kuwa ni watu wasio na elimu, wasio na maarifa, wakastaajabu, wakawatambua ya kwamba walikuwa pamoja na Yesu.”

 

Pampoja na ujasiri na ujazo wa nguvu za Roho Mtakatifu hebu jaribu kuwaza kama Petro na Yohana ndio wangekuwa wanafunzi wa kike tuchukulie Marim Magdalena na Salome wamesimamishwa mbele ya wanaume 70 wakihojiwa unapata picha gani?  Sisiemi kuwa wanawake hawawezi kuitetea imani kwa kiwango hiki, lakini hata wangerudi nyumbani huenda wangeambiwa na familia zao usijihusishe na mambo hata tena! Yesu alijua ni kwanini aliwatanguliza wanaume.

 

6.     Kuendeleza imani ya Wanaume ni kuendeleza Injili – Luka 10:1-6 “Basi, baada ya hayo Bwana aliweka na wengine, sabini, akawatuma wawili wawili wamtangulie kwenda kila mji na kila mahali alipokusudia kwenda mwenyewe. Akawaambia, Mavuno ni mengi, lakini watenda kazi ni wachache; basi mwombeni Bwana wa mavuno apeleke watenda kazi katika mavuno yake. Enendeni, angalieni, nawatuma kama wana kondoo kati ya mbwa-mwitu. Msichukue mfuko, wala mkoba, wala viatu; wala msimwamkie mtu njiani. Na nyumba yo yote mtakayoingia, semeni kwanza, Amani iwemo nyumbani humu;na akiwamo mwana wa amani, amani yenu itamkalia; la, hayumo, amani yenu itarudi kwenu.”

 

Kusudi kuu la huduma ya wanaume ni kuufikia ulimwengu, Kanisa ni lazima tuwafundishe wanaume kuitafuta sauti yao, na kuieneza injili, wanaume wengi hufikiri ya kuwa wao sio chombo sahihi cha kuipeleka injili au wanadhani hawana haki ya kumzungumzia Kristo tunahitaji kuwafundisha, tunahitaji kuwajengea ujasiri na tunahitaji kuwapa silaha ili wafanye umisheni, wamtumikie Mungu, watengeneze programu mbalimbali za kuonyesha upendo wa Kristo kwa wengine, wanaume wakiamka hakuna cha kuwazuia, Yesu kama haitoshi akafundisha darasa lingine tena la wanaume 70 ukiacha wale 12 na kisha akawatuma wawili wawili kuongeza kasi ya upelekaji habari njema kwa hiyo tunajifunza hapa kuwa jinsia hii haipaswi kupuuziwa hata kidogo katika maswala mazima ya kuipeleka injili kokote duniani!

 

7.     Wanaume wanapaswa kuwasaidia wanaume vijana -  Tito 2:6-10 “Vivyo hivyo na vijana waume uwaonye kuwa na kiasi; katika mambo yote ukijionyesha wewe mwenyewe kuwa kielelezo cha matendo mema, na katika mafundisho yako ukionyesha usahihi na ustahivu, na maneno yenye uzima yasiyoweza kuhukumiwa makosa, ili yule mwenye kupinga atahayarike, kwa kuwa hana neno baya la kunena juu yetu. Watumwa na wawatii bwana zao, wakiwapendeza katika mambo yote; wasiwe wenye kujibu, wasiwe waibaji; bali wauonyeshe uaminifu mwema wote, ili wayapambe mafundisho ya Mwokozi wetu Mungu katika mambo yote.”

 

Dunia inakwenda kwa kasi sana kama Kanisa litachelewa kimkakati kuwavuna wanaume, ni wazi kuwa pia tutachelewa kuwavuna vijana wa kiume au kizazi kijacho cha vijana wa kiume kitakosa walimu wazuri wa kuwafundisha, Paulo mtume mapema alikuwa amemuagiza Tito kuwa wanawake wazee wawafundishe wanawake vijana namna ya kuishi ona:-

 

Tito 2:3-5 “Vivyo hivyo na wazee wa kike wawe na mwenendo wa utakatifu; wasiwe wasingiziaji, wasiwe wenye kutumia mvinyo nyingi, bali wafundishao mema; ili wawatie wanawake vijana akili, wawapende waume zao, na kuwapenda watoto wao; na kuwa wenye kiasi, kuwa safi, kufanya kazi nyumbani mwao, kuwa wema, kuwatii waume zao wenyewe; ili neno la Mungu lisitukanwe.”

 

Kama wazee wa kike wanaweza kuwafunza wanawake vijana je vijana wa kiume watafunzwa na nani?  Vijana wanabadilika na wanakua na dunia inaenda kasi, wakati sisi tunashindwa kuwafikia wanaume na kuwasababisha wawe walezi wazuri kwa vijana agenda ya Ibilisi lazima itaelekezwa huko na je tutakua na kizazi cha namna gani, lazima kuweko na wanaume wakomavu walioiva kimaadili waweze kuwa msaada kwa kizazi kipya  cha wanaume vijana, tusipofanya nani atatufanyia, kama tunahitaji kanisa lenye nguvu basi tusisubiri muujiza ujitokeze lazima tufanye kazi ya kuwekeza kwa wanaume ili nao wawekeze kwa wanaume vijana, mwangalie Daudi alivyomuelekeza Suleimani

 

1Wafalme  2:1-4 “Basi siku ya kufa kwake Daudi ikakaribia, akamwusia Sulemani mwanawe, akasema,Mimi naenda njia ya ulimwengu wote; basi uwe hodari, ujionyeshe kuwa mwanamume; uyashike mausia ya Bwana, Mungu wako, uende katika njia zake, uzishike sheria zake, na amri zake, na hukumu zake, na shuhuda zake, sawasawa na ilivyoandikwa katika torati ya Musa, upate kufanikiwa katika kila ufanyalo, na kila utazamako ili Bwana afanye imara neno lake alilonena kwa habari yangu, akisema, Ikiwa watoto wako wataiangalia njia yao, wakienda mbele zangu kwa kweli, kwa moyo wao wote, na kwa roho yao yote, (akasema), hutakosa mtu katika kiti cha enzi cha Israeli.”                                           

Hitimisho!

1Timotheo 2:8 “Basi, nataka wanaume wasalishe kila mahali, huku wakiinua mikono iliyotakata pasipo hasira wala majadiliano.”

Kushughulika na wanaume sio program mpya ndani ya Kanisa bali ni swala la lazima kwa afya ya kanisa na usalama wa familia za Kikristo, Kama familia inaongozwa na wanaume katika mpango wa Mungu na mwanaume anafananishwa na Kristo katika itifaki ya uongozi wa Mungu je tunawezaje kuwaweka pembeni wanaume na kuwafikia wanawake kabla ya waume zao na Baba zao?  Je Mungu angelimtokea Sara na kumwambia toka wewe katika nchi yako wende katika nchi nitakayokuonyesha Je Abrahamu na Lutu, na mzee Tera nao wangelimfuata Sara?  Mwanaume ni kama sindano na mwanamke na familia ni kama uzi, pale sindano inapopita uzi utafuata, lakini ni vigumu sana kushina nguo kwa kuutanguliza uzi, Basi nataka wanaume wasalishe ni wito wa kutoa kipaumbele kwamba wanaume waokoke, wanaume wamtumikie Mungu, wanaume wakue kiroho, wanaume wawe watakatifu, wanaume wasalishe kila mahali! Wito huu ni  kwa wanaume kwamba wawe viongozi wa ibada kila mahali, waongoze maombi, waongoze ibada wasalishe, lakini sisemi kwamba wanawake hawawezi kufanya hilo, lakini mwanamke kufanya hilo ni mbadala.

 

Na. Rev. Innocent Samuel Kamote

Mkuu wa wajenzi mwenye Hekima