Wakolosai 4:15-18 “Wasalimuni ndugu walioko
Laodikia, na Nimfa, na kanisa lililo katika nyumba yake. Waraka huu ukiisha
kusomwa kwenu fanyeni kwamba usomwe katika kanisa la Walaodikia pia; na ule wa
Laodikia usomwe na ninyi. Mwambieni Arkipo, iangalie sana huduma ile uliyopewa
katika Bwana, ili uitimize. Salamu yangu mimi Paulo, kwa mkono wangu mwenyewe.
Kumbukeni kufungwa kwangu. Neema na iwe pamoja nanyi.”
Utangulizi:
Ni muhimu kufahamu kuwa katika
nyakati hizi tulizo nazo taarifa husambaa kwa haraka sana kwa njia ya simu, mitandao
ya kijamii, televisheni, redio, magazeti na kadhalika, Lakini nyakati za kanisa
la Kwanza taarifa zilikuwa zinasambaa kwa kupitia nyaraka tena katika mazingira
magumu sana, Paulo mtume aliyekuwa Gerezani alikuwa anataka nyaraka zake
anazoziandikia kanisa zisambae kutoka katika kanisa moja na kwenda kanisa
lingine kama njia ya kufikisha ujumbe wa injili na mafundisho ya Bwana, Kwa
hivyo barua zilikuwa zikizunguka kutoka kanisa moja kwenda kanisa lingine,
Paulo hakutaka Neno la Mungu libaki katika kanisa moja tu, badala yake alitaka
ziyafikie makanisa yote, Na huu ni ujumbe muhimu sana kwa kanisa la Mungu
katika nyakati zetu,Neno la Mungu halipaswi kuwa hatimiliki ya kanisa moja tu
na badala yake ujumbe wa neno la Mungu unapaswa kuwafikia watu wote Ona :-
Wakolosai 4:15-18 “Wasalimuni ndugu walioko
Laodikia, na Nimfa, na kanisa lililo katika nyumba yake. Waraka huu ukiisha
kusomwa kwenu fanyeni kwamba usomwe katika kanisa la Walaodikia pia; na ule wa
Laodikia usomwe na ninyi. Mwambieni Arkipo, Iangalie sana huduma ile uliyopewa
katika Bwana, ili uitimize. Salamu yangu mimi Paulo, kwa mkono wangu mwenyewe.
Kumbukeni kufungwa kwangu. Neema na iwe pamoja nanyi.”
Katika kifungu hiki cha msingi
cha neno la Mungu ambacho tunajifunza leo, tunasoma maelekezo ya Paulo Mtume
kwa kanisa la Kolosai kwamba waraka wao wahakikishe unasomwa katika kanisa la
Laodikia na ule wa Laodikia usomwe na wao, hii inatufundisha somo muhimu sana
ya kuwa Neno au ujumbe wa neno la Mungu unaotumiwa na Kanisa moja au aliopewa
mtumishi wa Mungu kwaajili ya Kanisa fulani, unaweza pia kutumiwa na Kanisa
lingine kwa makusudi ya kujengana,
kutiana moyo, kuhudumia mwili wa Kristo na kwaajili ya shughuli za kimaongozi, kwa
kufanya hivi kanisa litakuwa na umoja na litahitimu katika nia moja.
Waraka wa Kolosai unaweza kusomwa
na Laodikia na ule wa Laodikia unaweza kusomwa Kolosai, hii inatufundisha wazi
kuwa nyakati za kanisa la kwanza nyaraka za Paulo Mtume na huenda hata na za
mitume wengine zilisomwa vilevile katika makanisa mengine na hivyo ufunuo wa
hekima wa neno la Mungu na miongozo
mbalimbali ingeweza kuwa na faida na kusaidia kanisa lingine. Na sio hivyo tu
mafundisho ya mitume yangelisaidia Kanisa ulimwenguni kote kujenga umoja wa
kikanisa na ushirikiano, hii haitofautiani hata kidogo na swala la Paulo mtume
kumuagiza Timotheo kuhubiri kile alichokisikia kwake na kuwakabidhi watu
waaminifu watakaofaa kuwafundisha wengine:-
2Timotheo 2:2 “Na mambo yale uliyoyasikia
kwangu mbele ya mashahidi wengi, hayo uwakabidhi watu waaminifu watakaofaa
kuwafundisha na wengine.”
Kwa msingi huo tunajifunza hapa
kwamba waraka yaani ujumbe wa Mungu wa kanisa “A” unaweza pia kusomwa
“Kuhubiriwa” na Kanisa “B” na ule wa Kanisa “B” ukasomwa “Kuhubiriwa” na Kanisa “A”, Mungu anapomtumia
mtumishi wake kuleta ujumbe kwa Kanisa lake la mahali pamoja, ujumbe huo,
huweza kuwafaa watu wa Kanisa lingine, hiki ndicho tunachojifunza kutokana na
maelekezo ya Paulo mtume, Jambo kubwa la msingi ni mtumishi wa Mungu kukaa
katika hali ya maombi na kuutafasiri ujumbe anaojifunza kutoka kwa wengine
katika mazingira ya watu wa Kanisa lake, kwa utulivu huku ukimpa nafasi Roho
Mtakatifu kwa sababu yeye ndiye Mwalimu wetu Mkuu.
Na jambo hili linafaa zaidi kama
Kanisa au watu wa mahali hapo wanapitia changamoto zinazofanana kama ilivyokuwa
kwa Kolosai na Laodikia, aidha inaweza kuwa vema kufanya hivyo kwa sababu sio
kila mtu anaweza kuwa mpishi hata kama wote ni familia moja na tunakaa katika
nyumba moja, Mungu amewapa neema wengine kuwa na uwezo wa kuandaa jumbe
kutokana na mazingira ya utulivu waliyo nayo au karama ya ualimu waliyo nayo na
mwingine anaruhusiwa kutumia ikiwa ataona vyema kufanya hivyo na kama
itampendeza Roho Mtakatifu kwani Roho Mtakatifu ni mmoja pia. Kufanya hivyo sio
kufanya wizi wa kitaarifa “Plagiarism”
kwani ujumbe wa Mungu sio taarifa bali ni mafundisho kwa kanisa lote. Kwa sababu
hiyo Leo tutachukua muda kujifunza na kutafakari ujumbe wa somo hili lenye
kichwa “Waraka huu ukiisha kusomwa
kwenu!” kwa kuzingatia vipengele vitatu vofuatavyo:-
·
Waraka
huu ukiisha kusomwa kwenu!
·
Fanyeni
kwamba usomwe katika kanisa lingine.
·
Faida ya kushirikishana
ujumbe wa neno la Mungu.
Waraka huu ukiisha kusomwa kwenu!
Ni muhimu kufahamu kuwa katika Barua
yake kwa Wakolosai, Paulo mtume anawapa maagizo ya wazi kuhusu kushirikiana
waraka wake na Kanisa lingine la Laodikia. Maagizo haya yanatufundisha na kutuonyesha umuhimu wa kushirikiana ujumbe
wa neno la Mungu na makanisa mengine tofauti tofauti, kwani ujumbe huo una
umuhimu wa kipekee kwa Kanisa linapokuja swala la kushirikiana na kuhubiri neno
la Mungu, Kanisa ni mwili wa Kristo na kwa sababu hiyo uko umuhimu wa
kuhudumiana na ndivyo neno la Mungu linavyoagiza.
1Petro 4:10-11 “kila mmoja kwa kadiri
alivyoipokea karama, itumieni kwa kuhudumiana; kama mawakili wema wa neema
mbalimbali za Mungu. Mtu akisema, na aseme kama mausia ya Mungu; mtu akihudumu,
na ahudumu kwa nguvu anazojaliwa na Mungu; ili Mungu atukuzwe katika mambo yote
kwa Yesu Kristo. Utukufu na uweza una yeye hata milele na milele. Amina.”
Wakolosai, Walaodikia na
Hierapoli yalikuwa ni makanisa yaliyoanzishwa na Epafra katika Asia ndogo, Epafra ni moja ya watumishi wa Mungu
anayetajwa katika waraka wa Wakolosai na Filemoni, alikuwa ni muhubiri wa
injili aliyekuwa na umuhimu mkubwa sana katika Kanisa la Kolosai na ni wazi
kuwa alihusika kulianzisha Kanisa hilo pamoja na mengine yaliyokuwa Asia na
alikuwa akiwaombea sana Wakolosai, Walaodikia na Hierapoli, Lakini pia alikuwa
ni mtendakazi wa karibu sana wa Paulo mtume na waliwahi kufungwa pamoja naye
gerezani kwaajili ya injili. Ona:-
Wakolosai 4:12-13 “Epafra, aliye mtu wa
kwenu, mtumwa wa Yesu Kristo, awasalimu, akifanya bidii siku zote kwa ajili
yenu katika maombi yake, ili kwamba msimame wakamilifu na kuthibitika sana
katika mapenzi yote ya Mungu. Maana namshuhudia kwamba ana juhudi nyingi kwa
ajili yenu, na kwa ajili ya hao walioko Laodikia, na kwa ajili ya hao walioko
Hierapoli.”
Filemoni 1:23 “Na pamoja na hayo uniwekee
tayari mahali pa kukaa; maana nataraji ya kwamba kwa maombi yenu mtajaliwa
kunipata. Epafra, aliyefungwa pamoja nami katika Kristo Yesu, akusalimu;”
Paulo Mtume akiwa na Epafra
anaandika waraka kwa Wakolosai na huenda aliandika na waraka mwingine kwa
kanisa la Laodikia ambao kwa bahati mbaya hauko katika Biblia yetu leo au
inawezekana ulipotea lakini anawaagiza Wakolosai kuwa waraka aliowaandikia
wakiisha kuusoma wahakikishe unasomwa na watu wa Laodikia na ule wa Laodikia
usomwe pia na Wakolosai, kwa nini Paulo anatoa agizo hili?
1.
Paulo
alitaka watu washirikiane kweli ya injili
- Alifahamu kuwa ujumbe wake wa injili ulikuwa na umuhimu mkubwa kwa
ulimwengu mzima, alikuwa anatambua kuwa Kanisa ni mwili mmoja na kwa vile
waraka wake kwa Wakolosai ulikuwa na mafundisho ya msingi kumuhusu Yesu kama
kichwa cha Kanisa na kweli kuhusu wokovu alitamani waraka huo huo ufike
Laodikia ili kwamba mafundisho yake yaweze kuwafikiwa wakristo wengi Duniani na
wote wajengwe kuwa na imani moja, Paulo alifahamu kuwa neno la Mungu lina pumzi
ya Mungu na kwa sababu hiyo linafaa kwa mafundisho sio ya kanisa fulani tu kla mahali pamoja bali na makanisa mengine:-
2Timotheo
3:14-17 “Bali wewe ukae katika mambo yale
uliyofundishwa na kuhakikishwa, kwa maana unajua ni akina nani ambao ulijifunza
kwao; na ya kuwa tangu utoto umeyajua maandiko matakatifu, ambayo yaweza
kukuhekimisha hata upate wokovu kwa imani iliyo katika Kristo Yesu. Kila
andiko, lenye pumzi ya Mungu, lafaa kwa mafundisho, na kwa kuwaonya watu makosa
yao, na kwa kuwaongoza, na kwa kuwaadibisha katika haki; ili mtu wa Mungu awe
kamili, amekamilishwa apate kutenda kila tendo jema.”
2.
Paulo
mtume alitaka makanisa yote yakabiliane na mafundisho ya uongo – Makanisa
yote ya Kolosai na Laodikia yalikuwa yakikabiliwa na changamoto ya mafundisho
ya uongo yakiwemo yale ya Kiyahudi yanayochanganya kweli ya injili na sheria za
kiyahudi (Jewish legalism) na
mafundisho ya “Gnosticism” waliokazia
kuwa dhambi ni ujinga na wokovu unaletwa na ufahamu au maarifa, aidha pia watu
walikuwa wakifundisha maono na ndoto ambazo kimsingi hazikuwa kweli ya neno la
Mungu,Walifundisha kushika sabato, kuandama mwezi na baadhi ya maswala ya
sheria tofauti na kweli ya injili, Yalikuweko pia mafundisho yahusuyo kuutesa
mwili, msishike, msiguse wala msionje (Asceticism)
Paulo alitaka makanisa yote yapokee mafundisho safi na ya kweli yanayomzingatia
Kristo, sio hivyo tu Mitume walitaka mafundisho yao yaenezwe katika makanisa
yote na watu wayashike, na kama mtu haleti mafundisho hayo waliagiza
asikaribishwe, wala wasitamani kula naye maana kufanya hivyo ni kuunga mkono mafundisho
potofu. Adui wa Kolosai alikuwa ndiye adui wa Laodikia kwa hiyo kwa
kushirikiana nyaraka za kitume makanisa yote yangeimarika kwa fundisho sahihi.
Wakolosai
2:16-19 “Basi, mtu asiwahukumu ninyi katika vyakula
au vinywaji, au kwa sababu ya sikukuu au mwandamo wa mwezi, au sabato; mambo
hayo ni kivuli cha mambo yajayo; bali mwili ni wa Kristo. Mtu asiwanyang'anye
thawabu yenu, kwa kunyenyekea kwa mapenzi yake mwenyewe tu, na kuabudu malaika,
akijitia katika maono yake na kujivuna bure, kwa akili zake za kimwili; wala
hakishiki Kichwa, ambacho kwa yeye mwili wote ukiruzukiwa na kuungamanishwa kwa
viungo na mishipa, hukua kwa maongeo yatokayo kwa Mungu.”
2Yohana 1:7-10
“Kwa maana wadanganyifu wengi wametokea duniani,
wasiokiri ya kuwa Yesu Kristo yuaja katika mwili. Huyo ndiye yule mdanganyifu
na mpinga Kristo. Jiangalieni nafsi zenu msiyapoteze mliyoyatenda, bali mpokee
thawabu timilifu.Kila apitaye cheo, wala asidumu katika mafundisho ya Kristo,
yeye hana Mungu. Yeye adumuye katika mafundisho hayo, huyo ana Baba na Mwana
pia. Mtu akija kwenu, naye haleti mafundisho hayo, msimkaribishe nyumbani
mwenu, wala msimpe salamu.”
3. Paulo alitaka kanisa linie mamoja Kanisa ni
mwili mmoja – Ingawa Kanisa la Kolosai na Laodikia yalikuwa katika sehemu
tofauti au miji mbalimbali tofauti kushirikiana kwao nyaraka au mafundisho ya
mtume kulimaanisha kuwa Kanisa ni mwili mmoja, Paulo alilenga kuyafanya
makanisa haya kuwa ndugu na kutaka kuimarisha uhusiano katika ya kanisa moja na
jingine kwa hiyo kushirikiana mafundisho halikuwa jambo baya, Biblia
inapoelezea kuwa Kanisa ni mwili mmoja bado pia inaelezea ya kuwa lina viungo
vingi, kwa maana hiyo ingawa Kanisa ni moja lakini lina karama na utendaji
tofauti tofauti, lakini ingawa mwili ni mmoja
na una viungo vingi hiyo haimaanishi kwamba mwili unaweza kula chakula
tofauti tofauti kwaajili ya kila kiungo, chakula ni kimoja, kwa hiyo Kanisa ni
moja na utendaji ni tofauti, tunaujenga mwili ule ule!
1Wakorintho
12:12-27 “Maana kama vile mwili ni mmoja, nao una
viungo vingi, na viungo vyote vya mwili ule, navyo ni vingi, ni mwili mmoja;
vivyo hivyo na Kristo.Kwa maana katika Roho mmoja sisi sote tulibatizwa kuwa
mwili mmoja, kwamba tu Wayahudi, au kwamba tu Wayunani; ikiwa tu watumwa au
ikiwa tu huru; nasi sote tulinyweshwa Roho mmoja.Kwa maana mwili si kiungo
kimoja, bali ni vingi. Mguu ukisema, Kwa kuwa mimi si mkono, mimi si wa mwili;
je! Si wa mwili kwa sababu hiyo? Na sikio likisema, Kwa kuwa mimi si jicho,
mimi si la mwili; je! Si la mwili kwa sababu hiyo? Kama mwili wote ukiwa jicho,
ku wapi kusikia? Kama wote ni sikio ku wapi kunusa? Bali Mungu amevitia viungo
kila kimoja katika mwili kama alivyotaka. Lakini kama vyote vingekuwa kiungo
kimoja, mwili ungekuwa wapi? Lakini sasa viungo ni vingi, ila mwili ni mmoja.
Na jicho haliwezi kuuambia mkono, Sina haja na wewe; wala tena kichwa hakiwezi
kuiambia miguu, Sina haja na ninyi. Bali zaidi sana vile viungo vya mwili
vidhaniwavyo kuwa vinyonge zaidi vyahitajiwa zaidi. Na vile viungo vya mwili
vidhaniwavyo kuwa havina heshima, viungo vile twavipa heshima zaidi; na viungo
vyetu visivyo na uzuri vina uzuri zaidi sana. Kwa maana viungo vyetu vilivyo na
uzuri havina uhitaji; bali Mungu ameuungamanisha mwili, na kukipa heshima zaidi
kile kiungo kilichopungukiwa; ili kusiwe na faraka katika mwili, bali viungo
vitunzane kila kiungo na mwenziwe. Na kiungo kimoja kikiumia, viungo vyote
huumia nacho, na kiungo kimoja kikitukuzwa, viungo vyote hufurahi pamoja nacho.
Basi ninyi mmekuwa mwili wa Kristo, na viungo kila kimoja peke yake.”
4. Paulo Mtume alitaka kuweka sawa mtazamo wa
kitheolojia kuhusu ubora wa Kristo – Nyaraka yake ilikuwa inabeba mtazamo
sahihi wa ubora wa Yesu Kristo na sadaka yake ya upatanisho aliyoitoa msalabani,
Paulo anamuelezea Yesu Kristo kwa mtazamo wa juu sana akionyesha kuwa Yeye ni
Muumba wa vitu vyote na kuwa katika yeye unakaa utimilifu wote wa Mungu na kwa
sababu hiyo alitaka ujumbe huu ueleweke wazi kwa makanisa yote ambayo kimsingi
yalikuwa yanashirikiana eneo moja la kijiografia na hivyo ilikuwa ni wazi kuwa
mafundisho yanayoshusha heshima ya Kristo yangeweza kuyaathiri makanisa yote
mawili na zaidi hivyo kubadilishana nyaraka kungelifanya wawe na msimamo mmoja na
kauli moja na uhakika kutoka kwa mtume
Wakolosai
1:15-20 “naye ni mfano wa Mungu asiyeonekana,
mzaliwa wa kwanza wa viumbe vyote. Kwa kuwa katika yeye vitu vyote viliumbwa,
vilivyo mbinguni na vilivyo juu ya nchi, vinavyoonekana na visivyoonekana;
ikiwa ni vitu vya enzi, au usultani, au enzi, au mamlaka; vitu vyote viliumbwa
kwa njia yake, na kwa ajili yake. Naye amekuwako kabla ya vitu vyote, na vitu
vyote hushikana katika yeye. Naye ndiye kichwa cha mwili, yaani, cha kanisa;
naye ni mwanzo, ni mzaliwa wa kwanza katika wafu, ili kwamba awe mtangulizi
katika yote. Kwa kuwa katika yeye ilipendeza utimilifu wote ukae; na kwa yeye
kuvipatanisha vitu vyote na nafsi yake akiisha kufanya amani kwa damu ya
msalaba wake; kwa yeye, ikiwa ni vitu vilivyo juu ya nchi, au vilivyo mbinguni.”
Wakolosai
2:13-15 “Na ninyi mlipokuwa mmekufa kwa sababu ya
makosa yenu na kutokutahiriwa kwa mwili wenu, aliwafanya hai pamoja naye,
akiisha kutusamehe makosa yote; akiisha kuifuta ile hati iliyoandikwa ya
kutushitaki kwa hukumu zake, iliyokuwa na uadui kwetu; akaiondoa isiwepo tena,
akaigongomea msalabani; akiisha kuzivua enzi na mamlaka, na kuzifanya kuwa
mkogo kwa ujasiri, akizishangilia katika msalaba huo.
5. Paulo alikuwa na ufahamu kuwa ujumbe
anaouandika haukuwa kwaajili ya kanisa la mahali pamoja tu, ulikuwa pia
kwaajili ya sehemu nyingine, Hakuna kanisa ambalo linaweza kudai kuwa fundisho
walilonalo ni la kwao peke yao, wala muhubiri mmoja kudhani kuwa ujumbe
anaopewa na Roho Mtakatifu ni wa kwake tu, Nataka nikuhakikishie kuna wachoyo
wengi sana wana jumbe hawaandiki, wala hawazirushi katika mitandao ya kijamii
kwa sababu wanadhani ni za kwao tu na za kanisa lake la mahali pamoja au
wanataka kuzifanyia biashara “you cant
monopolize the Gospel as if it belongs
you alone” “huwezi kuhodhi injili kana kwamba ni mali yako pekee” Mungu
hajakuita kwaajili ya kanisa la mahali pamoja tu sidhani kama uko wito wa namna
hiyo Mungu ametuita kwaajili ya mataifa yote, unaporejea kwenye kanisa lako la
mahali pamoja umerudi tu kwenye nyumba yako, au kituo chako cha nyumbani lakini
linapokluja swala la injili sio ya mahali pamoja ni ya dunia nzima. Pailo mtume
alikuwa anafahamu asili ya witio wake kuwa jni wito kwa mataifa yote, na agizo
kuu pia limeagiza kwamba injili ihubiriwe ulimwenguni kote enendendi ulimwenguni
kote!
Matendo 9:15-16.
“Lakini Bwana akamwambia, Nenda tu; kwa maana huyu
ni chombo kiteule kwangu, alichukue Jina langu mbele ya Mataifa, na wafalme, na
wana wa Israeli. Maana nitamwonyesha yalivyo mengi yatakayompasa kuteswa kwa
ajili ya Jina langu.”
Warumi 11:13 “Lakini nasema na ninyi, mlio watu wa Mataifa. Basi, kwa
kadiri nilivyo mtume wa watu wa Mataifa, naitukuza huduma iliyo yangu, nipate
kuwatia wivu walio damu moja na mimi na kuwaokoa baadhi yao.”
Wagalatia
1:15-16 “Lakini Mungu, aliyenitenga tangu tumboni
mwa mama yangu, akaniita kwa neema yake, alipoona vema kumdhihirisha Mwanawe
ndani yangu, ili niwahubiri Mataifa habari zake; mara sikufanya shauri na watu
wenye mwili na damu;”
Mwanzo 12:1-3 “BWANA akamwambia Abramu, Toka wewe katika nchi yako, na
jamaa zako, na nyumba ya baba yako, uende mpaka nchi nitakayokuonyesha; nami
nitakufanya wewe kuwa taifa kubwa, na kukubariki, na kulikuza jina lako; nawe
uwe baraka;nami nitawabariki wakubarikio, naye akulaaniye nitamlaani; na katika
wewe jamaa zote za dunia watabarikiwa.”
Unaona Mungu anapomuita mtumishi wake hamuiti kwaajili ya
kanisa la mahali pamoja tu, kujidhania kuwa umeitwa kwaajili ya sehemu moja tu
ni kosa la kiufundi, wewe ni sauti ya Mungu kutoka pale ulipo kuelekea kila
mahali ulimwenguni, Mungu aliponiita mimi katika huduma hii, aliniambia nitakufanya
kuwa fundi mkuu utatengeneza matofali, kisha utawapa watu wataijenga nyumba
yangu kila mahali ulimwenguni, ndio maana ya mkuu wa wajenzi, tunaujenga mwili
wa Kristo, mtu akitumia jumbe zangu nafurahi sana kwa sababu kile ambacho Mungu
amenipa kinaenea duniani kote, na haya ndio mapenzi ya Mungu, na tangu nimeanza
kufanya hivyo sijawahi kupungukiwa na jumbe, Roho Mtakatifu amekuwa mwaminifu
akinipa Jumbe kila wakati kwaajili yenu, kwaajili ya mwili wa Kristo, zitumieni kama
Bwana anavyowaongoza, sijisikii vibaya watu wakihudumu na kuhubiri jumbe zangu
kwa sababu zimekuwa Baraka kubwa kila mahali ulimwenguni, zinawafikia watu
Msumbiji, Kongo, Kenya, Rwanda, Burundi, Marekani, Tanzania na maeneo
mbalimbali na hii ni furaha yangu! Na kama wewe unavyobarikiwa na kushangaa, na
mimi baada ya kumaliza kuandaa, huwa nabarikiwa na ninashangaa, kwamba hivi
mimi nawezaje kuwa natengeneza jumbe kali namna hii sio mimi ni Roho wa Mungu! Utukufu
ni wake!
Fanyeni kwamba usomwe katika kanisa lingine.
Kimsingi neno la Mungu
linaonyesha kuwa sio dhambi kwa watumishi wa Mungu kushirikishana mafundisho,
Neno la Mungu linaonyesha kuwa mafundisho yanapokelewa, yanahifadhiwa, na
yanapitishwa kutoka kizazi kimoja hata kizazi kingine na kwa sababu hiyo
tunajifunza kwamba sio dhambi kufundisha kile ulichofundishwa na ukawafundisha
watu wengine!
2Timotheo 2:2 “Na mambo yale uliyoyasikia
kwangu mbele ya mashahidi wengi, hayo uwakabidhi watu waaminifu watakaofaa
kuwafundisha na wengine.”
Kila mtumishi wa Mungu ana
wajibika kutunza maudhui sahihi ya mafundisho au maneno aliyoyasikia au kuyasoma
kutoka kwa wale waliojaliwa kuandika neno la Mungu, kufundisha kwa usahihi na
kwa uaminifu kile ulichojifunza kutoka
kwa wale unaowaamini au wale wenye imani moja na wewe, Mungu anachokitaka ni ile
kweli ilindwe, wakati huo huo tusiache kusoma na kuchimba maandiko na kujiachia
mbele za Roho Mtakatifu ili tuweze kupokea ufunuo sahihi unaoendana sawa na
neno la Mungu, tunatofautiana neema, mtazamo na uzoefu na karama au vipawa kwa
hiyo kila mmoja atafanya kwa kadiri ya neema aliyopewa, Kabla ya kuandika
injili yake Luka alikuwa amesoma injili zilizotangulia kuandikwa na nyingine,
kama injili ya Marko na Mathayo, hivyo yeye naye aliamua kuandika kwa jinsi
yake japokuwa injili zote zina lengo lile lile la kuelezea maisha na mafundisho
ya Bwana, Marko, Mathayo na Luka zinaitwa injili zinazofanana. “Synoptic Gospel” Lakini zikiwa na lengo
moja, hata hivyo Luka anaandika katika namna inayovutia zaidi na alifanya hivyo
baada ya kufanya utafiti wa kutosha ona:-
Luka 1:1-4 “Kwa kuwa watu wengi wametia
mikono kutunga kwa taratibu habari za mambo yale yaliyotimizwa katikati yetu,
kama walivyotuhadithia wale waliokuwa mashahidi wenye kuyaona, na watumishi wa
lile neno tokea mwanzo, nimeona vema mimi nami, kwa kuwa nimejitafutia usahihi
wa mambo hayo yote tangu mwanzo, kukuandikia kwa taratibu, Theofilo
mtukufu,upate kujua hakika ya mambo yale uliyofundishwa.”
Unaona Mathayo, Marko, Luka na
hata Yohana wote wanaandika habari za Yesu Kristo mafundisho yake na matendo
yake lakini kila mmoja akiwa na kionjo tofauti kwa aina yake, basi tuupeleke ujumbe wa injili kwa watu wote
kwa kadiri ya neema ya Mungu kila mtu kwa kionjo chake lakini lengo likiwa moja
kujenga mwili wa Yesu yaani kanisa.
Paulo anachoagiza sasa anataka
makanisa yote yashirikiane neno la Mungu, Mungu anaweza kuzungumza na Kanisa
lake kupitia ujumbe mmoja, Kanisa la Kolosai na Laodikia walipaswa kushirikiana
neno la Mungu lakini pia walifanya hivyo kwa makanisa mengine, ushirikiano wa
neno la Mungu ulipunguza gharama, ulisaidia kuwa na sauti ya umoja, kujilinda
na mafundisho ya uongo, Kanisa kuwa na fundisho lililo sahihi kwa pamoja, kwa hiyo
Kanisa la Kolosai linapokea Waraka wa Paulo na kanisa la Laodikia linapokea
waraka wa Paulo, Kisha Laodikia wanawashirikisha Kolosai na Kolosai
wanawashirikisha Laodikia, wote wanapata kopi na wote wanakuwa salama, huu ndio
mpango na makusudi ya Mungu.
Wakolosai 4:15-18 “Wasalimuni ndugu walioko
Laodikia, na Nimfa, na kanisa lililo katika nyumba yake. Waraka huu ukiisha
kusomwa kwenu fanyeni kwamba usomwe katika kanisa la Walaodikia pia; na ule wa
Laodikia usomwe na ninyi. Mwambieni Arkipo, iangalie sana huduma ile uliyopewa
katika Bwana, ili uitimize. Salamu yangu mimi Paulo, kwa mkono wangu mwenyewe.
Kumbukeni kufungwa kwangu. Neema na iwe pamoja nanyi.”
Faida ya kushirikishana ujumbe wa neno la Mungu.
Wakristo wanaposhirikiana neno la
Mungu kuna faida kadhaa zinajitokeza katika mwili wa Kristo zinaweza kuwepo
faida nyingi sana lakini kikubwa wote tunahitimu katika nia moja na kunena
mamoja, kukuza imani yetu pamoja, kukua kiroho pamoja, kujilinda katika imani
kwa pamoja na kutokutofautiana kwa kiwango kikubwa kati ya Kanisa moja na
lingine, kimisimamo na kimafundisho.
1Wakorintho 1:10-13. “Basi ndugu, nawasihi,
kwa jina la Bwana wetu Yesu Kristo, kwamba nyote mnene mamoja; wala pasiwe
kwenu faraka, bali mhitimu katika nia moja na shauri moja. Kwa maana, ndugu
zangu, nimearifiwa habari zenu na wale walio wa nyumbani mwa Kloe, ya kwamba
iko fitina kwenu. Basi, maana yangu ni hii, ya kwamba kila mtu wa kwenu kusema,
Mimi ni wa Paulo, na, Mimi ni wa Apolo, na, Mimi ni wa Kefa, na, Mimi ni wa
Kristo. Je! Kristo amegawanyika? Je! Paulo alisulibiwa kwa ajili yenu? Au je!
Mlibatizwa kwa jina la Paulo?”
1Petro 2:2-5 “Kama watoto wachanga
waliozaliwa sasa yatamanini maziwa ya akili yasiyoghoshiwa, ili kwa hayo mpate
kuukulia wokovu; ikiwa mmeonja ya kwamba Bwana ni mwenye fadhili. Mmwendee
yeye, jiwe lililo hai, lililokataliwa na wanadamu, bali kwa Mungu ni teule,
lenye heshima. Ninyi nanyi, kama mawe yaliyo hai, mmejengwa mwe nyumba ya Roho,
ukuhani mtakatifu, mtoe dhabihu za roho, zinazokubaliwa na Mungu, kwa njia ya
Yesu Kristo.”
Wakolosai 1:26-28 “siri ile iliyofichwa
tangu zamani zote na tangu vizazi vyote, bali sasa imefunuliwa kwa watakatifu
wake; ambao Mungu alipenda kuwajulisha jinsi ulivyo utajiri wa utukufu wa siri
hii katika Mataifa, nao ni Kristo ndani yenu, tumaini la utukufu ambaye sisi
tunamhubiri habari zake tukimwonya kila mtu, na kumfundisha kila mtu katika
hekima yote, tupate kumleta kila mtu mtimilifu katika Kristo”.
Ukiacha kuhitimu katika nia moja,
kuukulia wokovu kwa viwango vinavyoendana, kuwa watumilifu kama Kristo, vile
vile Kanisa tunaweza kujihami na mafundisho ya uongo yanayoingia kwa kasi
hususani katika nyakati hizi za mwisho, Kanisa la Kolosai liliingiliwa na
mafundisho ya uongo ambayo kama wao walitahadharishwa ingelikuwa rahisi kwa
Kanisa la Laodikia pia kuchukua tahadhari mapema kabla hayajawakuta.
Wakolosai 2:6-8 “Basi kama mlivyompokea
Kristo Yesu, Bwana, enendeni vivyo hivyo katika yeye; wenye shina na wenye
kujengwa katika yeye; mmefanywa imara kwa imani, kama mlivyofundishwa; mkizidi
kutoa shukrani. Angalieni mtu asiwafanye mateka kwa elimu yake ya bure na
madanganyo matupu, kwa jinsi ya mapokeo ya wanadamu, kwa jinsi ya mafundisho ya
awali ya ulimwengu, wala si kwa jinsi ya Kristo. Maana katika yeye unakaa
utimilifu wote wa Mungu, kwa jinsi ya kimwili.”
Unaona kwa tahadhari kama hii
basi uongo unadhibitiwa mapema, wakristo wanaweza kushauriana na kutiana moyo,
na umoja wa makanisa unaimarika na mwili wa Kristo unajengwa
Inarahisisha kuenea kwa injili, Paulo mtume alikuwa kizuizini,
alikuwa amefungwa lakini neno la Mungu halifungwi, Paulo angeliweza kama mtume
kuufikisha ujumbe katika makanisa hata bila yaye ye kufika na injili ingeenea na ingeenea kwa usahihi,
injili inawafikia watu wengi zaidi, kila Kanisa linafanyika kituo cha injili, Kanisa
linaimarika, makanisa yanazaliwa, imani inajengwa, Paulo alitambua ya kuwa ana
kitu na kitu hicho kinatakiwa kuwafikia watu wengi, akiwa amefungwa angewezaje
kuufikisha ujumbe ni kwa kuandika, kuishirikisha injili kila mahali ni agizo la
Kristo
Marko 16:15-16 “Akawaambia, Enendeni
ulimwenguni mwote, mkaihubiri Injili kwa kila kiumbe. Aaminiye na kubatizwa
ataokoka; asiyeamini, atahukumiwa.”
1Petro 3:15 “Mwe tayari siku zote kumjibu
kila mtu awaulizaye habari za tumaini lililo ndani yenu; lakini kwa upole na
kwa hofu.”
Warumi 1:1-6 “Paulo, mtumwa wa Kristo Yesu,
aliyeitwa kuwa mtume, na kutengwa aihubiri Injili ya Mungu;ambayo Mungu
amekwisha kuiahidi kwa kinywa cha manabii wake katika maandiko matakatifu;
yaani, habari za Mwanawe, aliyezaliwa katika ukoo wa Daudi kwa jinsi ya
mwili,na kudhihirishwa kwa uweza kuwa Mwana wa Mungu, kwa jinsi ya roho ya
utakatifu, kwa ufufuo wa wafu, Yesu Kristo Bwana wetu; ambaye katika yeye
tulipokea neema na utume ili mataifa yote wapate kujitiisha kwa imani, kwa ajili
ya jina lake; ambao katika hao ninyi mmekuwa wateule wa Yesu Kristo;”
Hitimisho:
Kwa hiyo tunajifunza ya kuwa
nyakati za Kanisa la Kwanza mitume walishirikisha watu wote neno la Mungu na
mafundisho yao, baadae nyaraka hizo zilikuswanywa pamoja na kufanyika neno la
Mungu yaani Biblia tuliyo nayo, hata hivyo Biblia inahitaji utaalamu
kuitafasiri na sio watu wote wanaweza lakini wale walioitwa kuwa walimu wanaweza
kufanya huduma yao kwa bidii na kuwasaidia wakristo kuifahamu kweli ya neno la
Mungu kwa jumbe zao, kwa hiyo ni vema ujumbe huu ukawafikia makanisa yote
endapo utabaini kuwa unaweza kuwasaidia na jumbe nyinginezo zote, waraka huu
ukiisha kusomwa kwenu, fanyeni kwamba usomwe katika Kanisa lingine na faida
yake utaiona Bwana atupe neema, kumfundisha kila mtu neno la Mungu ili injili
iweze kuwafikia watu wote kwa utukufu wa Mungu Baba mwenyewe
Warumi 12:4-8 “Kwa kuwa kama vile katika
mwili mmoja tuna viungo vingi, wala viungo vyote havitendi kazi moja; Vivyo
hivyo na sisi tulio wengi tu mwili mmoja katika Kristo, na viungo, kila mmoja
kwa mwenzake. Basi kwa kuwa tuna karama zilizo mbalimbali, kwa kadiri ya neema
mliyopewa; ikiwa unabii, tutoe unabii kwa kadiri ya imani; ikiwa huduma, tuwemo
katika huduma yetu; mwenye kufundisha, katika kufundisha kwake; mwenye kuonya,
katika kuonya kwake; mwenye kukirimu, kwa moyo mweupe; mwenye kusimamia kwa
bidii mwenye kurehemu, kwa furaha.”
Wakolosai 4:16-18. “Waraka huu ukiisha
kusomwa kwenu fanyeni kwamba usomwe katika kanisa la Walaodikia pia; na ule wa
Laodikia usomwe na ninyi.Mwambieni Arkipo, Iangalie sana huduma ile uliyopewa
katika Bwana, ili uitimize. Salamu yangu mimi Paulo, kwa mkono wangu mwenyewe.
Kumbukeni kufungwa kwangu. Neema na iwe pamoja nanyi.”
Na Rev. Innocent Samuel Kamote
Mkuu wa wajenzi mwenye hekima
.jpg)

