1Petro 5:2 “Nawasihi wazee walio kwenu,
mimi niliye mzee, mwenzi wao, na shahidi wa mateso ya Kristo, na mshirika wa
utukufu utakaofunuliwa baadaye; lichungeni kundi la Mungu lililo kwenu, na
kulisimamia, si kwa kulazimishwa, bali kwa hiari kama Mungu atakavyo; si kwa
kutaka fedha ya aibu, bali kwa moyo. Wala si kama wajifanyao mabwana juu ya
mitaa yao, bali kwa kujifanya vielelezo kwa lile kundi.”
Utangulizi
Moja ya majukumu ya huduma ya
kichungaji, ni pamoja na kulichunga kundi na kulisimamia, Neno kulichunga kundi
na kulisimamia katika kiyunani yanatumika maneno mawili “Poimainō”
na “Episkopeō” ambayo kwa kiingereza yanatafasirika kama
“Feed” na “look deligently” ambayo maana yake kwa Kiswahili ni kulisha na kuchunga “look deligently” “Carefully examine” “seek with total dedication” kufanya
uangalizi makini, kuchunguza kwa makini, kutafuta kwa kujidhabihu, kwa msingi
huo huduma ya kichungaji sio kuwalisha kondoo peke yake lakini pia kuwachunga
yaani kuchunguza kile wanachopitia, wana ugonjwa gani wanapitia changamoto gani
kisha kuzitatua kwa upendo hapo ndipo linapokuja swala la kufanya ushauri
nasihi, au ushauri wa kisaikolojia ingawa kazi ya ushauri wa kichungaji ni
zaidi ya ushauri wa kisaikolojia kwa sababu kuna ukaribu sana na maswala ya nafsi na roho.Kazi ya ushauri wa kichungaji
ni kazi ya kufariji kwa changamoto wanazopitia watu wa Mungu pamoja na kutafuta
suluhu kwa pamoja katika ile changamoto
anayopitia mtu husika.
Ayubu 2:11-13 “Basi ikawa hao rafikize
Ayubu watatu walipopata habari ya mabaya hayo yote yaliyomfikilia, wakaja kila
mtu kutoka mahali pake; nao ni Elifazi Mtemani, na Bildadi Mshuhi, na Sofari
Mnaamathi; wakapatana pamoja ili waende kumlilia Ayubu na kumtuliza moyo. Basi
walipovua macho yao, nao wakali mbali, wasimtambue, wakainua sauti zao na
kulia; kila mmoja akararua joho yake, wakarusha mavumbi juu ya vichwa vyao
kuelekea mbinguni. Kisha wakaketi nchi pamoja naye muda wa siku saba, mchana na
usiku, wala hapana mmoja aliyenena naye neno lo lote; kwa maana waliona ya kuwa
mashaka yake aliyo nayo ni makuu mno.”
Ayubu alipopatwa na mabaya,
Rafiki zake walitoka kwa kusudi la kusaidia kubeba pamoja naye maumivu yake na
kumfariji na kujadiliana naye kwa pamoja ili yamkini waweze kufikia suluhu ya
kifalsafa ya swali kubwa linaloulizwa na wanadamu wanapopitia changamoto nini
sababu ya mateso na kwa nini yanipate mimi, kufanya huduma ya aina hii ni
sehemu ya huduma ya kichungaji ambayo wahudumu, watendakazi, wanafunzi na wenye
hekima tunapaswa kuifanya pia kwaajili ya kuwabebea mizigo kondoo wa Bwana
wanaopitia changamoto mbalimbali. Huduma hii ni ya malezi, huduma hii ni ya uangalizi,
huduma hii ni ya ulinzi dhidi ya kondoo, huduma hii ni ushauri, na kutia moyo
Wagalatia 6:1-2 “Ndugu zangu, mtu
akighafilika katika kosa lo lote, ninyi mlio wa Roho mrejezeni upya mtu kama
huyo kwa roho ya upole, ukijiangalia nafsi yako usije ukajaribiwa wewe
mwenyewe. Mchukuliane mizigo na kuitimiza hivyo sheria ya Kristo.”
Tutajifunza somo hili ushauri wa
kichungaji kwa kuzingatia vipengele vitatu muhimu vifuatavyo:-
- Maana ya Huduma ya ushauri wa
Kichungaji
- Umuhimu wa huduma ya ushauri wa
kichungaji
- Misingi ya Ushauri wa Kichungaji
Maana ya Huduma ya ushauri wa Kichungaji
Ushauri wa kichungaji ni mfumo maalumu wa huduma ya kisaikolojia
unaotumia njia za kiroho na kisaikolojia kwaajili ya kumtia mtu moyo kiakili
ili kumuwezesha mtu huyo kuchukuliana na mazingira ya changamoto ngumu
inayomkabili na kuponya majeraha ya kihisia ambayo kwa kawaida inaathiri
maendeleo ya kimwili, kiroho na kiakili, Kimsingi njia za kisaikolojia zinaweza
kutumika kumponya mwanadamu kiakili na ndio maana wako wanasaikolojia
wanaofanya kazi za ushauri hata hivyo huduma ya kichungaji ya ushauri ina nguvu
zaidi kwa sababu haiishii katika akili pekee bali huenda mpaka katika roho na
kuleta ufumbuzi wenye manufaa, kwa hiyo ushauri wa kichungaji sio tiba ya
kitabibu, wala sio ushauri wa kisaikolojia, bali ni huduma inayolenga kuleta
uponyaji wa ndani na kujenga mwelekeo mwema wa maisha, Na ndio maana katika
sifa za Yesu Kristo yeye pia anaitwa Msahuri wa ajabu unaona!
Isaya 9:6-7 “Maana kwa ajili yetu mtoto
amezaliwa, Tumepewa mtoto mwanamume; Na uweza wa kifalme utakuwa begani mwake;
Naye ataitwa Jina Lake, Mshauri wa ajabu, Mungu mwenye nguvu, Baba wa milele,
Mfalme wa amani. Maongeo ya enzi yake na amani Hayatakuwa na mwisho kamwe,
Katika kiti cha enzi cha Daudi na ufalme wake; Kuuthibitisha na kuutegemeza Kwa
hukumu na kwa haki, Tangu sasa na hata milele. Wivu wa Bwana wa majeshi ndio
utakaotenda hayo.”
Sio hivyo tu Roho Mtakatifu
katika utendaji wake kamili, moja ya shughuli anayoifanya ni pamoja na ushauri
nasihi
Isaya 11:1-4 “Basi litatoka chipukizi
katika shina la Yese, na tawi litakalotoka katika mizizi yake litazaa matunda.
Na roho ya Bwana atakaa juu yake, roho ya hekima na ufahamu, roho ya shauri na
uweza, roho ya maarifa na ya kumcha Bwana; na furaha yake itakuwa katika kumcha
Bwana; wala hatahukumu kwa kuyafuata ayaonayo kwa macho yake, wala hataonya kwa
kuyafuata ayasikiayo kwa masikio yake; bali kwa haki atawahukumu maskini, naye
atawaonya wanyenyekevu wa dunia kwa adili; naye ataipiga dunia kwa fimbo ya
kinywa chake, na kwa pumzi ya midomo yake atawaua wabaya.”
Huduma ya ushauri wa kichungaji
huwasaidia watu kihisia, kiroho, na kimaadili na hufanyika kwa kutumia neno la
mungu na hekima inayowekwa kwetu na Roho Mtakatifu kwa sababu yeye ndiye
anayeyajua mambo ya roho ya mwanadamu na pia anayajua mambo ya Mungu kwa hiyo
mtu anayefanya kazi ya ushauri wa kiroho anapaswa kuwa amejazwa Roho Mtakatifu
kwaajili ya huduma hii na utumishi huu
1Wakorintho 2:10-14 “Lakini Mungu
ametufunulia sisi kwa Roho. Maana Roho Huchunguza yote, hata mafumbo ya Mungu.
Maana Ni nani katika binadamu ayajuaye mambo ya binadamu ila roho ya binadamu
iliyo ndani yake? Vivyo hivyo na mambo ya Mungu hakuna ayafahamuye ila Roho wa
Mungu. Lakini sisi hatukuipokea roho ya dunia, bali Roho atokaye kwa Mungu,
makusudi tupate kuyajua tuliyokirimiwa na Mungu. Nayo twayanena, si kwa maneno
yanayofundishwa kwa hekima ya kibinadamu, bali yanayofundishwa na Roho,
tukiyafasiri mambo ya rohoni kwa maneno ya rohoni. Basi mwanadamu wa tabia ya
asili hayapokei mambo ya Roho wa Mungu; maana kwake huyo ni upuzi, wala hawezi
kuyafahamu, kwa kuwa yatambulikana kwa jinsi ya rohoni.”
Kupitia huduma ya ushauri wa
kichungaji Bwana Yesu aliweza kumsaidia kimaadili mwanamke msamaria ambaye
kimsingi alikuwa anaishi maisha ya kikahaba huku akichukuwa waume za watu, na
kuishi katika usumbufu, wa kisaikolojia, alikuwa akichota maji saa za mchana
muda ambao wanawake wengine walikuwa wameacha kwenda kuchota maji, alijihukumu
mwenyewe kutokana na maisha ya ukahaba,
japo alikuwa na ufahamu fulani kuhusu kuabudu lakini haikuwa katika njia
sahihi, Yesu alipokutana naye alimshauri mambo ya ajabu ambayo yaliweza kabisa
kugeuza maisha yake na maisha ya watu wa mji mzima wa Samaria
Yohana 4:4-26 “Basi akafika kunako mji wa
Samaria, uitwao Sikari, karibu na lile shamba ambalo Yakobo alimpa Yusufu
mwanawe.Na hapo palikuwa na kisima cha Yakobo. Basi Yesu, kwa sababu amechoka
kwa safari yake, akaketi vivi hivi kisimani. Nayo ilikuwa yapata saa sita.
Akaja mwanamke Msamaria kuteka maji. Yesu akamwambia, Nipe maji ninywe. Kwa
maana wanafunzi wake wamekwenda mjini kununua chakula. Basi yule mwanamke
Msamaria akamwambia, Imekuwaje wewe Myahudi kutaka maji kwangu, nami ni
mwanamke Msamaria? (Maana Wayahudi hawachangamani na Wasamaria.) Yesu akajibu,
akamwambia, Kama ungaliijua karama ya Mungu, naye ni nani akuambiaye, Nipe maji
ninywe, ungalimwomba yeye, naye angalikupa maji yaliyo hai. Yule mwanamke
akamwambia, Bwana, huna kitu cha kutekea, na kisima ni kirefu; basi umeyapata
wapi hayo maji yaliyo hai? Je! Wewe u mkubwa kuliko baba yetu, Yakobo,
aliyetupa kisima hiki, naye mwenyewe akanywa maji yake, na wanawe pia, na
wanyama wake? Yesu akajibu, akamwambia, Kila anywaye maji haya ataona kiu tena;
walakini ye yote atakayekunywa maji yale nitakayompa mimi hataona kiu milele;
bali yale maji nitakayompa yatakuwa ndani yake chemchemi ya maji, yakibubujikia
uzima wa milele. Yule mwanamke akamwambia, Bwana, unipe maji hayo, nisione kiu,
wala nisije hapa kuteka. Yesu akamwambia, Nenda kamwite mumeo, uje naye hapa.
Yule mwanamke akajibu, akasema, Sina mume. Yesu akamwambia, Umesema vema, Sina
mume; kwa maana umekuwa na waume watano, naye uliye naye sasa siye mume wako;
hapo umesema kweli. Yule mwanamke akamwambia, Bwana, naona ya kuwa u nabii!
Baba zetu waliabudu katika mlima huu, nanyi husema ya kwamba huko Yerusalemu ni
mahali patupasapo kuabudia.Yesu akamwambia, Mama, unisadiki, saa inakuja ambayo
hamtamwabudu Baba katika mlima huu, wala kule Yerusalemu.Ninyi mnaabudu
msichokijua; sisi tunaabudu tukijuacho; kwa kuwa wokovu watoka kwa Wayahudi.
Lakini saa inakuja, nayo sasa ipo, ambayo waabuduo halisi watamwabudu Baba
katika roho na kweli. Kwa maana Baba awatafuta watu kama hao wamwabudu. Mungu
ni Roho, nao wamwabuduo yeye imewapasa kumwabudu katika roho na kweli.Yule
mwanamke akamwambia, Najua ya kuwa yuaja Masihi, (aitwaye Kristo); naye
atakapokuja, yeye atatufunulia mambo yote.Yesu akamwambia, Mimi ninayesema
nawe, ndiye.”
Ni kupitia huduma ya ushauri wa
kichungaji Yesu aliweza kufanikiwa kubadilisha tabia na ufahamu wa kiimani kwa
mwanamke Msamaria na Wasamaria wote waliokuja kumsikiliza baada ya ushuda wa
kufunguliwa kwa mwanamke huyu, Yako mambo ambayo maombi na maombezi pekee hayatoshi
kukamilisha uponyaji wa mtu lakini kupitia ushauri tunaweza kuwafikia watu wa
Mungu na kuwasaidia wakapona kiakili kiroho na kisaikolojia, haya yanaweza
kufanyika kupitia huduma ya ushauri, kusikiliza, kuuliza maswali na kuelekeza
katika ukweli wa mambo!
Umuhimu wa huduma ya ushauri wa kichungaji.
Kimsingi kila mwanadamu anahitaji
ushauri, hakuna mwanadamu anajitosheleza yeye mwenyewe hata kama mwanadamu huyo
yuko karibu na Mungu, kuna wakati mtu mwingine anaweza kuliona jambo kwa jinsi
nyingine au katika pembe nyingine na akalitolea ufumbuzi, kwa mfano Musa
alikuwa akifanya huduma ya ushauri na watu wengi walikuwa wakimuendea, na akawa
akiwashauri na kuwaamua, hata hivyo pamoja na haya aliyokuwa akiyafanya kuhani
mkuu wa Midian Yethro alikuja na kumshauri kitu cha kufanya ili yeye na watu
anaowahudumia waweze kuwa salama
Kutoka 18:13 -24 “Asubuhi yake Musa akaketi
ili awapishie hukumu watu; na hao watu wakasimama kumzunguka Musa tangu asubuhi
hata jioni. Mkwewe Musa alipoyaona yote aliyowafanyia watu, akasema, Ni jambo
gani hili uwatendealo hao watu? Kwani wewe kuketi hapo peke yako, na watu wote
kusimama kwako tangu asubuhi hata jioni? Musa akamwambia mkwewe, Ni kwa sababu
watu hunijilia mimi wapate kumwuliza Mungu; wakiwa na neno, hunijilia; nami
naamua kati ya mtu na mwenziwe, nami nawajuvisha amri za Mungu, na sheria zake.
Mkwewe Musa akamwambia, Jambo hili ufanyalo si jema. Huna budi utadhoofika
wewe, na hawa watu walio pamoja nawe pia; maana jambo hili ni zito mno kwako;
huwezi wewe kulitenda peke yako. Sikiza sasa neno langu, nitakupa shauri, na
Mungu na awe pamoja nawe; uwe wewe kwa ajili ya watu mbele ya Mungu, nawe
umletee Mungu maneno yao; nawe utawafundisha zile amri na sheria, nawe
utawaonyesha njia ambayo inawapasa kuiendea, na kazi ambayo inawapasa kuifanya.
Zaidi ya hayo utajipatia katika watu hawa watu walio na uwezo, wenye kumcha
Mungu, watu wa kweli, wenye kuchukia mapato ya udhalimu; ukawaweka juu yao,
wawe wakuu wa maelfu, na wakuu wa mia, na wakuu wa hamsini, na wakuu wa kumi; nao
wawaamue watu hawa sikuzote; kisha, kila neno lililo kubwa watakuletea wewe,
lakini kila neno dogo wataliamua wenyewe; basi kwako wewe mwenyewe utapata
nafasi zaidi, nao watauchukua huo mzigo pamoja nawe. Kwamba utafanya jambo
hili, na Mungu akikuagiza hivyo, basi utaweza kusimama wewe, na watu hawa wote
nao watakwenda mahali pao kwa amani.Basi Musa akasikiza neno la mkwewe,
akayafanya yote aliyokuwa amemwambia.”
Tunajifunza hapo kwamba kila
mwanadamu anahitaji ushauri, Musa alikuwa nabii mkubwa sana na mwenye
kuzungumza na Mungu uso kwa uso, Lakini alishauriwa na mkwewe namna njema na
bora ya kutumika, ni ukweli uliokuwa wazi kuwa Musa peke yake angeumia kuifanya
kazi hiyo kwali aliifanya asubuhi mpaka jioni, sisi nasi kama watenda kazi
hatuiwezi kuiacha kazi hii mikononi mwa wachungaji pekee ni lazima kundi la
watu wa makumi, na mamia na maelelfu waluiofunza kama hivi katika shule ya
huduma wahusike pia katika kutoa ushauri wa kichungaji kwa washirika wetu kwani
sio kila jambo linaweza kuponywa kutokea madhabahuni, watu wanahitaji
kusikilizwa, kuuliza maswali na kujibiwa na kufunguliwa pia kwa njia ya
mazungumzo na kusaidiwa sana kiroho huduma hii ni muhimu sana kwa sababu
1. Inawalinda kondoo wasipotee – kuna
makundi makubwa ya watu makanisani yaani katika makanisa ya kiroho wanapotea kimya
kimya sababu kubwa ni kukaa na changamoto na kukosa msaada na ushauri wa
kichungaji unaoweza kuwatatulia shida zao na kuwarejeza ni kama vile laiti
wangelipata mtu wa kuwasikiliza kwa kina!
Mathayo 18:12-14 “Mwaonaje? Mtu akiwa na kondoo mia, mmoja akampotea, je!
Hawaachi wale tisa na tisini, akaenda milimani, na kumtafuta yule aliyepotea?
Hata akipata kumwona, amin, nawaambia, amfurahia huyo zaidi, kuliko wale tisa
na tisini wasiopotea.Vivyo hivyo haipendezi mbele za Baba yenu aliye mbinguni
kwamba mmoja wa wadogo hawa apotee.”
2. Ushauri wa kichungaji husaidia kuleta
uponyaji wa ndani – wako watu wengi ambao wana maumivu ya ndani, hawaumwi
na hawana mapepo, lakini wana maumivu moyoni kwaajili ya mambo yaliyopita,
maumivu ya kihisia, na kadhalika ambao wanahitaji uponyaji wa ndani ambao
unaweza kuletwa kwao kwa ushauri wa kichungaji kama watumishi wa Mungu tunajihusisha
sana na kondoo wa Bwana, Mchungaji biashara yake ni watu, kwa hiyo mtumishi wa
Mungu wa ngazi yoyote ile na wa kundi la kiwango chochote kile huduma ya
ushauri wa kichungaji inatuhusu, watu wakipata mchungaji wa namna hii
watamuamini na kuona kweli unajishughulisha na mambo yao kuchunga ni pamoja na
kujishughulisha na maisha ya waamini wetu na kuwasikiliza na kuwaganga wapone
Matendo 20:28 “Jitunzeni nafsi zenu, na lile kundi lote nalo, ambalo
Roho Mtakatifu amewaweka ninyi kuwa waangalizi ndani yake, mpate kulilisha
kanisa lake Mungu, alilolinunua kwa damu yake mwenyewe.”
Zaburi 23:1-6 “Bwana ndiye mchungaji wangu, Sitapungukiwa na kitu.
Katika malisho ya majani mabichi hunilaza, Kando ya maji ya utulivu huniongoza.
Hunihuisha nafsi yangu; na kuniongoza Katika njia za haki kwa ajili ya jina
lake. Naam, nijapopita kati ya bonde la uvuli wa mauti, Sitaogopa mabaya; Kwa
maana Wewe upo pamoja nami, Gongo lako na fimbo yako vyanifariji. Waandaa meza
mbele yangu, Machoni pa watesi wangu. Umenipaka mafuta kichwani pangu, Na
kikombe changu kinafurika. Hakika wema na fadhili zitanifuata Siku zote za maisha
yangu; Nami nitakaa nyumbani mwa Bwana milele.”
3. Kusaidia kondoo kufanya maamuzi sahihi – Washirika kama
ilivyo kwa kila mtu anahitaji wakati fulani kufanya maamuzi, ulimwengu wa roho
una tabia ya kusubiria wakati wa maamuzi kwa sababu wakati huo nafsi ya
mwanadamu inaweza kuingia katika uamuzi chanya au uamuzi hasi, kwa sababu hiyo
hakuna wakati Muhimu duniani kama wakati wa kufanya maamuzi, kwa sababu hiyo
wakati mwingine wanadamu hutafuta mahali sahihi wanapoweza kusaidwa kufanya
maamuzi sahihi, kuna maamuzi ya kifamilia, maisha, ndoa, utumishi, kazi, utatuzi
wa migogoro, uchaguzi wa mwenza, ununuzi wa vitu vya thamani na kadhalika
Zaburi 32:8-10 “Nitakufundisha na kukuonyesha njia utakayoiendea;
Nitakushauri, jicho langu likikutazama. Msiwe kama farasi wala nyumbu, Walio
hawana akili. Kwa matandiko ya lijamu na hatamu Sharti kuwazuia hao, au
hawatakukaribia. Naye mtu mwovu ana mapigo mengi, Bali amtumainiye Bwana
fadhili zitamzunguka.”
4. Ushauri wa kichungaji ni ulinzi dhidi ya
matukio mabaya – Kwa kutoa ushauri wa kichungaji waamini wanalindwa dhidi
ya hisia, usalama, muongozo wa kiroho na kisaikolojia, kanuni na kuinua
nia vyote inakuwa ngao kwa kila mtu, na
kuwalinda dhidi ya uharibifu, skendo na kadhalika kwa kuwapa maelekezo sahihi
ya kimaandiko au muongozo wa Mungu, kusahihisha, kulinda na hatari, na
mafundisho au Imani potofu
Matendo 27:21-25 “Na walipokuwa wamekaa wakati mwingi bila kula chakula,
Paulo akasimama katikati yao, akasema, Wanaume, iliwapasa kunisikiliza mimi na
kutokung'oa nanga huko Krete, na kupata madhara haya na hasara hii. Sasa
nawapeni shauri, iweni na moyo mkuu, kwa maana hapana hata nafsi mmoja miongoni
mwenu atakayepotea, ila merikebu tu. Kwa maana usiku huu wa leo malaika wa
Mungu yule ambaye mimi ni wake, naye ndiye nimwabuduye, alisimama karibu nami,
akaniambia, Usiogope, Paulo, huna budi kusimama mbele ya Kaisari; tena, tazama,
Mungu amekupa watu wote wanaosafiri pamoja nawe.Basi, wanaume, changamkeni; kwa
sababu namwamini Mungu, ya kwamba yatakuwa vile vile kama nilivyoambiwa.”
5. Hujenga uaminifu, upendo na uwajibikaji
– Huduma ya ushauri wa kichungaji inajenga uwajibikaji wa wahudumu wa injili
kwa washirika wao, lakini pia unapofanikisha mambo yao unajijengea kuaminiwa,
na kuunda upendo wa kweli, huduma hii inaashiria kuwa unajali watu, unapenda
watu, unaheshimu watu, na unawathamini kwa hiyo washirika watafunguka zaidi kwa
kanisa lao na wahudumu wa kanisa lao kwani utawatunzia pia siri zao na kuwaongoza
kwa hekima bila kuathiri amani yao kwa hiyo huu ndio moyo wa huduma ya
kichungaji
1Wakorintho 13:4-8 “Upendo huvumilia, hufadhili; upendo hauhusudu; upendo
hautakabari; haujivuni; haukosi kuwa na adabu; hautafuti mambo yake; hauoni
uchungu; hauhesabu mabaya; haufurahii udhalimu, bali hufurahi pamoja na kweli;
huvumilia yote; huamini yote; hutumaini yote; hustahimili yote.Upendo haupungui
neno wakati wo wote; bali ukiwapo unabii utabatilika; zikiwapo lugha, zitakoma;
yakiwapo maarifa, yatabatilika.”
Misingi ya Ushauri wa Kichungaji
Huduma ya ushauri wa kichungaji
ina miiko yake na misingi yake ya kimaadili ni huduma ya muhimu sana lakini
inahitaji uangalifu mkubwa kwa sababu hiyo inahitaji sana hekima na maarifa na
akili, na ndio maana makanisa mengi yameshindwa kuwa na huduma za namna hii na
kuwaacha watu wahangaike kwa mataifa kutafuta ushauri, kwa wanasaikolojia, na
washauri wengine, Mungu anatarajia watu wa ndani katika kanisa wawe na hekima
ya kufanya maamuzi na mashauri badala ya maswala ya kikanisa kupelekwa kwa
mataifa, Hata hivyo kama viongozi na watenda kazi katika kanisa watakosa hekima
hii na kuzingatia misingi ya ushauri wa kichungaji watu wanaweza kusema heri
kwenda kwa mataifa na sisi tutakuwa tumeshindwa kutimiza wajibu wetu
ipaswavyo;-
1Wakorintho 6:1-6 “Je! Mtu wa kwenu akiwa
ana daawa juu ya mwenzake athubutu kushitaki mbele ya wasio haki, wala si mbele
ya watakatifu? Au hamjui ya kwamba watakatifu watauhukumu ulimwengu? Na ikiwa
ulimwengu utahukumiwa na ninyi, je! Hamstahili kukata hukumu zilizo ndogo?
Hamjui ya kuwa mtawahukumu malaika, basi si zaidi sana mambo ya maisha haya?
Basi, mkiwa na mahali panapohukumiwa mambo ya maisha haya, mwawaweka kuwa
waamuzi hao waliohesabiwa kuwa si kitu; katika kanisa? Nasema hayo nipate
kuwatahayarisha. Je! Ndivyo, kwamba kwenu hakuna hata mtu mmoja mwenye hekima,
awezaye kukata maneno ya ndugu zake? Bali mwashitakiana, ndugu kwa ndugu, tena
mbele yao wasioamini.”
Mambo yafuatayo yazingatiwe basi na kila mtenda kazi, mhudumu,
mwanafunzi, na wenye hekima katika kanisa
1. Kusikiliza – anapokuja mtu mwenye
majanga yake kwaajili ya kutafuta ushauri wa kichungaji ni vema sana
akasikilizwa, mtu mmoja alisema ni kama Mungu ametupa masikio mawili na mdomo
mmoja ili tusikilize zaidi kuliko kusema sana, kwa hiyo tujitie nidhamu
kumsikiliza mtu ajielezee bila kuwa na kiherehere cha kuzungumza au kujibu kwa
haraka ama kudhani kuwa tuna ufumbuzi wa haraka ni muhimu kusikiliza kwanza.
Yakobo 1:19 “Hayo mnajua, ndugu zangu wapenzi. Basi kila mtu na awe
mwepesi wa kusikia, bali si mwepesi wa kusema; wala kukasirika;”
2. Usiri – watu wanachukizwa wakati
mwingine na ushauri wa kichungaji hasa katika makanisa ya kipentekoste kwa
sababu wakati mwingine unatoka tu katika
chumba cha ushauri tayari habari zako watu wanazo, au unatolewa habari zako
madhabahuni kwenye bomba kama mfano wakati wa mahubiri labda linaweza kuachwa
kutajwa jina lako tu hii ni swala linasikitisha sana ni lazima tuwe na moyo
wenye kutunza siri au mafriji yanayogandisha, si vizuri siri za mshauriwa
zikatoka nje au kufanyiwa masimulizi au mifano utoaji wa siri huharibu huduma
hii, kama madaktari wanavyoficha siri tunza siri za watu, hatupendi kusikia
nimekuambia tafadhali usije ukamwambia mtu, na mwingine unamsikia aliyeniambia
kaniambia nisimwambie mtu lakini wakati huo huo habari zimeenea
Mithali 11:12-14 “Asiye na akili humdharau mwenziwe; Bali mtu aliye na
ufahamu hunyamaza. Mwenye kitango akisingizia hufunua siri; Bali mwenye roho ya
uaminifu husitiri mambo.Pasipo mashauri taifa huanguka; Bali kwa wingi wa
washauri huja wokovu.”
Mithali 25:2 “Ni utukufu wa Mungu kuficha jambo; Bali ni utukufu wa
mfalme kuchunguza jambo.”
3. Zingatia mahusiano – Ni vema kujihami
kwa sababu katika kutoa ushauri wa kichungaji kumejitokeza changamoto za aina
nyingi na ndio maana watumishi wengine wa Mungu hawapendi kufanya huduma hii,
jilinde, mlinde na anayekuja kushauriwa msikae faragha sana, epukeni ukaribu wa
kimwili na kihisia usiofaa, zingatia kulinda uhusiano na jinsia tofauti kwa
tahadhari kubwa ili kujiepusha na kashfa na skendo za aina mbalimbali, Paulo amabye hakuwa na mke alifanya
kazi pamoja na Prisila na Akila waliokuwa mume na mke kwaajili ya kutunza
ushuhuda ili neno la Mungu lisitukanwe!
1Wathesalonike
5:22-23. ”jitengeni na ubaya wa kila namna. Mungu
wa amani mwenyewe awatakase kabisa; nanyi nafsi zenu na roho zenu na miili yenu
mhifadhiwe mwe kamili, bila lawama, wakati wa kuja kwake Bwana wetu Yesu Kristo.”
Waefeso 5:3-5 “Lakini uasherati usitajwe kwenu kamwe, wala uchafu wowote
wala wa kutamani kama iwashtahilivyo watakatifu, wala aibu wala maneno ya
upuuzi wala ubishi; hayo hayapendezi bali afadhali kushukuru, maana neno hili
mnalijua hakika ya kwamba hakuna mwasherati wala mchafu wala mwenye tamaa,
ndiye mwabudu sanamu, aliye na urithi katika ufalme wa Kristo na Mungu”
Matendo 18:18 “Baada ya hayo Paulo akazidi kukaa huko siku nyingi, kisha
akaagana na ndugu akaabiri kwenda Shamu; na Prisila na Akila wakaenda pamoja
naye, alipokwisha kunyoa kichwa chake huko Kenkrea; maana alikuwa ana nadhiri.”
4. Usiutumie ushauri kwa manufaa binafsi – kutokana
na huduma hizi kuwa adimu na huduma ya kichungaji ya ushauri kutolewa bure
watumishi wengi wa Mungu wamekuwa wakijinufaisha kifedha na kuwatoza watu fedha
nyingi hasa wale wanaotaka kuwaona uso kwa uso kwaajili ya Ushauri, kamwe
usitumie huduma hii kama njia ya kujinufaisha, kuchukua rushwa, na kuteka watu
kingono, au kuwatawala watu, kuwaendesha na kudhibiti nafsi zao hilo jambo sio
la haki, aidha ni muhimu kujilinda
kwa sababu wakati mwingine yule unayempa ushauri anaweza kuwa ni majibu ya
tatizo lako binafsi wewe mtoa ushauri, na mkajikuta manajaribiwa kwa kuwa majibu
ya kila mmoja kwa mwenzake.
2Wakorintho 2:15-17
“Kwa maana sisi tu manukato ya Kristo, mbele za
Mungu, katika wao wanaookolewa, na katika wao wanaopotea; katika hao wa pili
harufu ya mauti iletayo mauti; katika hao wa kwanza harufu ya uzima iletayo uzima.
Naye ni nani atoshaye kwa mambo hayo? Kwa maana sisi si kama walio wengi,
walighoshio neno la Mungu; bali kama kwa weupe wa moyo, kama kutoka kwa Mungu,
mbele za Mungu, twanena katika Kristo.”
5. Tambua mipaka ya kihuduma - Unapokuwa
umesikiliza vya kutosha wale tunaowahudumia unaweza kugundua kuwa kuna maswala
mengine huwezi kuwa na majibu nayo, hayo yanaweza kuwa yanahitaji madaktari au
wana saikolojia, kwa hiyo unaweza kumuelekeza mtu aende sehemu sahihi kulingana
na changamoto yake na kufanya hivyo sio kushindwa kwa sababu sisi
tunashughulikia maswala ya kiroho, Yesu aliweza kumfufua Lazaro lakini swala la kumfungua sanda haikuwa kazi
yake, na Yesu aliweza kumfufua binti Yairo lakini kazi ya kumpa chakula haikuwa
ya kwake, unapotoa ushauri fanya eneo lako ambalo kimsingi ni la kiroho na
kisaikolojia kwa sehemu na mengine kama yako nje ya uwezo wako mpeleke
kunakohusika, mfano Menopouse na Andrepouse Ukomo wa hedhi na changamoto zake
na ukomo wa uzazi kwa wanaume yanaweza kuzungumzwa na wataalamu wa afya
Yohana 11:41-44 “Basi wakaliondoa lile jiwe. Yesu akainua macho yake juu,
akasema, Baba, nakushukuru kwa kuwa umenisikia. Nami nalijua ya kuwa wewe
wanisikia sikuzote; lakini kwa ajili ya mkutano huu wanaohudhuria nalisema
haya, ili wapate kusadiki kwamba ndiwe uliyenituma. Naye akiisha kusema hayo,
akalia kwa sauti kuu, Lazaro, njoo huku nje. Akatoka nje yule aliyekufa,
amefungwa sanda miguuni na mikononi, na uso wake amefungwa leso. Naye Yesu
akawaambia, Mfungueni, mkamwache aende zake.”
Marko 5:39-43 “Alipokwisha kuingia, akawaambia, Mbona mnafanya ghasia na
kulia? Kijana hakufa, bali amelala tu.Wakamcheka sana. Naye alipokwisha kuwatoa
nje wote, akamtwaa babaye yule kijana na mamaye, na wale walio pamoja naye,
akaingia ndani alimokuwamo yule kijana. Akamshika mkono kijana, akamwambia,
Talitha, kumi; tafsiri yake, Msichana, nakuambia, Inuka. Mara akasimama yule
kijana, akaenda; maana alikuwa amepata umri wa miaka kumi na miwili. Mara
wakashangaa mshangao mkuu. Akawaonya sana, mtu asijue habari ile; akaamuru
apewe chakula.”
6. Uwe muadilifu – huduma ya ushauri
inahitaji uwe mwadilifu, wakati mwingine kile unachikishauri inawezekana
kikasababisha uwe majibu ya yule unayemshauri, mfano anakuja mwanamke mzuri tu
na anakuletea kesi kuwa mumewe hamridhishi kwenye tendo la ndoa, na wewe
mhudumu una changamoto nyumbani unanyimwa tendo la ndioa na mkeo au nawe
huridhishi unajikuta majibu ya changamoto yako yako kwa mteja wako bila
uadilifu binafsi huduma hii inaweza kukuweka pasipo, au unaweza kushauri kwa
uchungu mfano anakuja mwanaume ambaye ananyimwa tendo la ndoa na wewe ni
muhanga wa kunyimwa unaweza kujikuta mnaungana kuwachukia wanawake uadilifu ni
nyenzo muhimu, jilinde na mjaribu, jilinde na tuhuma jilinde na kusingiziwa,
1Timotheo 3:2-5 “Basi imempasa askofu awe mtu asiyelaumika, mume wa mke
mmoja, mwenye kiasi na busara, mtu wa utaratibu, mkaribishaji, ajuaye
kufundisha; si mtu wa kuzoelea ulevi, si mpiga watu; bali awe mpole; si mtu wa
kujadiliana, wala asiwe mwenye kupenda fedha; mwenye kuisimamia nyumba yake
vema, ajuaye kutiisha watoto katika ustahivu; (yaani, mtu asiyejua kuisimamia
nyumba yake mwenyewe, atalitunzaje Kanisa la Mungu?)”
Wagalatia 6:1-2 “Ndugu zangu, mtu akighafilika katika kosa lo lote, ninyi
mlio wa Roho mrejezeni upya mtu kama huyo kwa roho ya upole, ukijiangalia nafsi
yako usije ukajaribiwa wewe mwenyewe. Mchukuliane mizigo na kuitimiza hivyo
sheria ya Kristo.”
Hitimisho
Huduma hii ni ya moyo, ni huduma ya usikivu, ni huduma ya
huruma, ni huduma ya kujali, ni huduma ya uaminifu, ni ulinzi wa kondoo wa
Bwana hatuna budi kumuomba Mungu atupe moyo wa huruma ili tuwahudumie watu wake.
uwe na watu karibu ili kama mshauriwa atakuwa na pepo kuwe na msaada wa
kihuduma wakati pepo zinakemewa na kutolewa ikiyajua hayo heri wewe ukiyatenda
!
Yeremia 3:15 “nami nitawapa ninyi wachungaji wanipendezao moyo wangu,
watakaowalisha kwa maarifa na fahamu.”
Na. Rev. Innocent
Samuel Kamote
Mkuu wa wajenzi
mwenye Hekima


