Kutoka 1:8-12. “Basi akainuka mfalme mpya
kutawala Misri, asiyemjua Yusufu. Akawaambia watu wake, Angalieni, watu wa wana
wa Israeli ni wengi tena wana nguvu kuliko sisi. Haya! Na tuwatendee kwa akili,
wasije wakaongezeka; tena, ikitokea vita, wao nao wasije wakashikamana na adui
zetu na kupigana nasi, na kutoka katika nchi hii. Basi wakaweka wasimamizi juu
yao wawatese kwa mizigo yao. Nao wakamjengea Farao miji ya kuwekea akiba,
Pithomu na Ramesesi. Lakini kwa kadiri ya walivyowatesa ndivyo walivyoongezeka
na kuzidi kuenea. Nao walichukiwa kwa sababu ya wana wa Israeli.”
Utangulizi:
Ni muhimu ikafahamika tena na
tena kwa wanadamu wote Duniani kuwa kusudi la Mungu kwa mtu yeyote duniani
haliwezi kubatilishwa na mtu awaye yote hata kama mtu huyo ana nguvu kuliko
tunavyofikiri, Stori ya wana wa Israeli Kutoka Misri inaanza kwa kuinuka kwa
mfalme mpya ambaye kwa ujeuri tu alijifanya hafahamu Historia na mchango wa Yusufu katika nchi ya Misri,
Kwa hofu yake dhidi ya Waisraeli anapanga njama na kukusudia kuwatesa na
kuwakandamiza Israel ili ikiwezekana waangamie na kupotelea mbali, Lakini jambo
la kushangaza ni kuwa “Kadiri walivyowatesa
ndivyo walivyoongezeka”, Kanuni ya Mungu hapa inatenda kazi ya kuwa huwezi
kumlaani Mtu ambaye Mungu amembariki, na huwezi kumshusha mtu ambaye Mungu
amemuinua.
Hesabu 23:5-8 “Bwana akatia neno katika
kinywa chake Balaamu, akasema, Umrudie Balaki; ukaseme maneno haya. Akarudi
kwake, na tazama, amesimama karibu na sadaka yake ya kuteketezwa, yeye na wakuu
wote wa Moabu pamoja naye. Akatunga mithali yake, akasema, Balaki amenileta
kutoka Aramu, Mfalme wa Moabu kutoka milima ya mashariki, Njoo! Unilaanie
Yakobo, Njoo! Unishutumie Israeli. Nimlaanije, yeye ambaye Mungu hakumlaani?
Nimshutumuje, yeye ambaye Bwana hakumshutumu?”
Mamlaka ya Mungu ni kubwa kuliko mamlaka za kibinadamu, uweza wa Mungu ni mkuu kuliko uweza wa wenye kuonea, Rehema za Mungu ni kubwa kuliko matendo ya wenye dhuluma, Njama za kibinadamu haziwezi kushindana na mpango kazi na mpango mkakati wa Mungu, Hofu ya mfalme wa Misri ilikuwa kubwa kwa sababu Mungu alikuwa amewabariki Israel na wakawa wengi na wenye nguvu kuliko Wamisri, si kuwa watu hao walikuwa waovu bali walikuwa wanastawi na ustawi wao ukawa ni tishio kubwa kwa wamisri na mfalme wao, lakini katika namna ya kushangaza sana Kadiri ya walivyowatesa ndivyo walivyoongezeka!, tutajifunza somo hili kwa kuzingatia vipengele muhimu vitatu vifuatavyo:-
·
Jinsi
Baraka za Mungu zinavyokufanya uwe tishio.
·
Kadiri ya
walivyowatesa ndivyo walivyoongezeka!.
·
Kusudi la
Mungu haliwezi kufutwa na wivu wa wanadamu.
Jinsi Baraka za Mungu zinavyokufanya uwe tishio.
Ni muhimu kufahamu kuwa Israel
kushuka kule Misri halikuwa tukio la bahati mbaya bali ulikuwa ni mpango wa
Mungu, Mungu alimweleza wazi rafiki yake Abrahamu kuwa uzao wake utashuka Misri
na kukaa huko kwa muda mrefu na kisha baadae angeliwapandisha katika inchi ya
Kanaani nchi ambayo Bwana alikuwa amemwapia Ibrahimu ya kuwa atampa yeye na
uzao wake.
Mwanzo 15:13-16 “BWANA akamwambia Abramu,
Ujue hakika ya kwamba uzao wako utakuwa mgeni katika nchi isiyo yake,
watawatumikia watu wale, nao watateswa muda wa miaka mia nne. Hata na taifa
lile, watakaowatumikia, nitawahukumu; baadaye watatoka na mali mengi. Lakini
wewe utakwenda kwa baba zako kwa amani, utazikwa katika uzee mwema. Na kizazi
cha nne kitarudi hapa, maana haujatimia uovu wa Waamori bado.”
Kwa hiyo aliyopitia Israeli
ulikuwa ni mpango na makusudi ya Mungu, Mungu alikuwa amefanya agano na
Ibrahimu na Isaka na Yakobo kuhusu wao na uzao wao, kwa sababu hiyo
isingelikuwa rahisi agano hilo kuvunjika kwa sababu yoyote ile, Mungu
aliwabariki sana na kuwapa mafanikio
makubwa, Kimsingi Israel hawakuwa watu waovu walikuwa wema na watu wa Mungu
hata hivyo walichukiwa kwa sababu Mungu alikuwa amewabariki, na Mungu aliwapa
ustawi mkubwa, hata leo hii Mkono wa Mungu unapokuwa juu yako kwa sababu zozote
zile mafanikio yako yatazaa wivu, chuki na upinzani na wakati mwingine
majaribio ya kipumbavu ya watu kutaka kukuangamiza hili ni jambo la kawaida kwa
mujibu wa mafundisho ya kibiblia Baraka zako zitakufanya uogopwe na kuwavutia
maadui wenye wivu
Kutoka 1:7-10 “Na wana wa Israeli walikuwa
na uzazi sana, na kuongezeka mno, na kuzidi kuwa wengi, nao wakaendelea na
kuongezeka nguvu; na ile nchi ilikuwa imejawa na wao. Basi akainuka mfalme mpya
kutawala Misri, asiyemjua Yusufu. Akawaambia watu wake, Angalieni, watu wa wana
wa Israeli ni wengi tena wana nguvu kuliko sisi. Haya! Na tuwatendee kwa akili,
wasije wakaongezeka; tena, ikitokea vita, wao nao wasije wakashikamana na adui
zetu na kupigana nasi, na kutoka katika nchi hii.”
Unaona! Mungu anapokupenda na
kuwekeza kitu cha ziada ndani yako watu hawapendi na hawawezi kufurahi na kwa
sababu hiyo watatumia mamlaka zao na nguvu zao na hila zao na ubinadamu wao
kukuletea upinzani au kujaribu kuharibu mpango wa Mungu ulioko ndani yako
lakini jambo la ajabu ni kuwa kila wakati watakapojaribu kufanya hivyo wewe
utaongezeka na hutazoofika lakini wao kwa upande wao watadhoofika na kupata
hofu kubwa zaidi, kanuni hii imejitokeza mara kadhaa katika maisha ya watu wa
Mungu na kwako sio jambo la ajabu ona;-
Mwanzo 26:12-16 “Isaka akapanda mbegu
katika nchi ile, akapata mwaka ule vipimo mia kwa kimoja, BWANA akambariki. Na
mtu huyu akawa mkuu, akazidi kusitawi, hata akawa mkuu sana. Akawa na mali ya
kondoo, na mali ya ng'ombe, na watumwa wengi. Hao Wafilisti wakamhusudu. Na
vile visima vyote walivyochimba watumwa wa baba yake, siku za Ibrahimu babaye,
Wafilisti walikuwa wamevifukia, wakavijaza kifusi. Abimeleki akamwambia Isaka,
Utoke kwetu, maana wewe una nguvu sana kuliko sisi.”
1Samuel 18:6-9 “Hata ikawa, walipokuwa
wakienda, hapo Daudi aliporudi baada ya kumwua yule Mfilisti, wanawake wakatoka
katika miji yote ya Israeli, kwa kuimba na kucheza, ili kumlaki mfalme Sauli;
wakatoka na matari, na shangwe, na vinanda. Nao wale wanawake wakaitikiana
wakicheza, wakasema, Sauli amewaua elfu zake, Na Daudi makumi elfu yake. Basi
Sauli akaghadhibika sana, na maneno haya yakamchukiza; akasema, Wamempa Daudi
makumi elfu, na mimi wamenipa elfu tu; kuna nini tena awezayo kupata, isipokuwa
ni ufalme? Sauli akamwonea Daudi wivu tangu siku ile.”
Daniel 6:1-5 “Ilimpendeza Dario kuweka juu
ya ufalme maliwali mia na ishirini, wawe juu ya ufalme wote; na juu yao akaweka
wakubwa watatu, na Danieli alikuwa mmoja wao; ili maliwali hawa watoe hesabu
kwao, mfalme asipate hasara. Basi Danieli huyo alipata sifa kuliko wakubwa na
maliwali, kwa kuwa roho bora ilikuwa ndani yake; naye mfalme akaazimu kumweka
juu ya ufalme wote. Basi mawaziri na maamiri wakatafuta sana kupata sababu za
kumshitaki Danieli kwa habari za mambo ya ufalme; lakini hawakuweza kuona
sababu wala kosa; kwa maana alikuwa mwaminifu, wala halikuonekana kosa wala
hatia ndani yake. Ndipo wale watu wakasema, Hatutapata sababu ya kumshitaki
Danieli huyo, tusipoipata katika mambo ya sheria ya Mungu wake.”
Unaona mkono wa Mungu unapokuwa
juu yako, watu wanaweza kukuogopa, wanaweza kukufukuza, wanaweza kukuonea wivu
na wanaweza kutengeneza majungu dhidi yako, kama uko au unazungukwa na watu wa
mwilini hata mnaosali pamoja kanisani na wengine wanaweza kuwa na cheo kikubwa
kabisa kuliko wewe na lakini ukuu wa Mungu ulioko ndani yako unawogopesha,
unaonekana kama unaweza kuwa na madhara kwao hata kama huna lengo wala nia ya
kuwadhuru, wataogopa sana wakiona mioyo ya watu inaambatana nawe, watajaribu
kukufukia na kukukandamiza na hata kukusema ili uonekane kuwa wewe sio kitu
lakini kama mkono wa Mungu uko juu yako na wewe ni uzao wa agano lake
hawatakuweza na kadiri wanavyokutesa ndivyo unavyozidi kuongezeka na kuwa tishio
Kadiri ya walivyowatesa ndivyo walivyoongezeka!
Biblia inatuonyesha kanuni ambayo
iko kinyume na mtazamo wa kibinadamu, kadiri Mfalme wa Misri alivyokuwa
akifanya mpango wa kuwaangamiza Israel ndivyo Israel walivyozidi kuongezeka na
kustawi sana, ingetegemewa kuwa mbinu ya chuki na njama za Farao zingeliweza
kuwa na mafanikio makubwa na kuwafanya Israel kuwa dhaifu lakini hata hivyo
Mungu alifanya kinyume na matazamio yake, Mungu hugeuza laana kuwa baraka,
Waliwatesa ili wasiongezeke lakini Israel waliongezeka, waliwaumiza ili wasiwe
na nguvu lakini wakawa na nguvu zaidi, waliwadhalilisha lakini Mungu aliwaheshimisha,
walitaka kuwaua watoto wao lakini wanawake walizaa kwa uhodari, waliwakandamiza
lakini Mungu aliwainua Mungu alisimamia kusudi lake na Agamo lake alilofanya na
Ibrahimu.
Mwanzo 12:1-3 “BWANA akamwambia Abramu,
Toka wewe katika nchi yako, na jamaa zako, na nyumba ya baba yako, uende mpaka
nchi nitakayokuonyesha; nami nitakufanya wewe kuwa taifa kubwa, na kukubariki,
na kulikuza jina lako; nawe uwe baraka; nami nitawabariki wakubarikio, naye
akulaaniye nitamlaani; na katika wewe jamaa zote za dunia watabarikiwa.”
Mpango wa Mungu kwa maisha yetu
uko Dhahiri kiimani na kihistoria na kivitendo, Mungu anapokuwa amekusudia
kukubariki hakuna mtu anaweza kuufuta mpango huo, wakati watu wanataka kukushusha
Mungu atakupandisha kwa nguvu, hakuna mbinu, njama wala silaha au hila itakayoweza
kufanikiwa dhidi yako, Mungu atakubariki kupitiliza na utatoboa kimaisha utafanikiwa
na utapanda juu sana na adui zako watakuogopa kila watakapojaribu kukushambulia
watashambuliwa vikali na nguvu iletayo wokovu juu yako na kimsingi utaongezeka,
mfano huu ni Dhahiri katika maisha yetu na katika taifa la Kiyahudi kwa sababu
ya agano lake alilofanya na baba yetu
Ibrahimu
Mwaka 1967 mwezi June kuanzia
Tarehe 5 mpaka Tarehe 10 pale mashariki ya kati palitokea vita kali sana kati
ya Muungano wa mataifa ya kiarabu ikiwemo Misri, Jordani, na Syria na baadaye
Iraq dhidi ya Israel, mataifa haya yalikuwa na mpango kabambe wa siri wa
kuishambulia Israel na kuifuta katika ramani ya dunia kila taifa lilijiandaa
thabiti kuhakikisha kuwa watu wakiamka asubuhi hakuna Israel, Katika namna ya
kushangaza Israel iliwapiga vikali sana jirani zake na kupata ushindi wa ajabu
ulioifanya Israel kuongezeka kiramani mara dufu zaidi, Israel iliendesha
oeperesheni iliyoitwa kwa kiingereza “Operation
Focus” na kuipiga vibaya Misri na
kuiteka ghuba ya Sinai, Jodran ilipigwa vibaya na kuachilia ukanda wa Gaza,
huku Syria ikipoteza Milima ya Golan pamoja na hayo Misri ilipoteza ndege vita
zaidi ya 338 masaa ya mwanzo tu ya vita, Sryria ikipoteza ndege vita 73 na Jordani
ndege 29 Iraq ambao nao walijiunga baadae kwa kusudi la kujihami walipoteza
ndege 29 Israel ikaibuka mshindi wa vita ile huku ikiwa imeongeza mipaka yake
yote ikiwa na udhibiti kamili wa maeneo hayo waliposhambuliwa zaidi
walijiongeza! Unaona
Kwa nini nimetoa mfano huo mtu wa
Mungu usiogope kadiri adui zako wanavyojaribu kukusumbua na kukuundia zengwe
wewe utazidi kuongezeka na hofu kubwa itawakalia wao, wewe utaendelea kustawi
kama Israel inavyostawi leo, hakuna mtu atakayeweza kusimama mbele yako siku
zote za maisha yako, wanadamu wanaweza kupinga kusudi la Mungu lilioko ndani
yako lakini kamwe hawawezi kuufikia mpango wa Mungu ulioko juu yako kwa sababu
wewe umebarikiwa! Kadiri wanavyopigana na wewe ndivyo na wewe unavooongezeaka!
Isaya 54:14-17 “Utathibitika katika haki;
utakuwa mbali na kuonewa, kwa maana hutaogopa; na mbali na hofu, kwa maana
haitakukaribia. Tazama, yamkini watakusanyana; lakini si kwa shauri langu. Watu
wo wote watakaokusanyana juu yako wataanguka kwa ajili yako. Tazama, nimemwumba
mhunzi avukutaye moto wa makaa, akatoa silaha kwa kazi yake; nami nimemwumba
mharibu ili aharibu. Kila silaha itakayofanyika juu yako haitafanikiwa na kila
ulimi utakaoinuka juu yako katika hukumu utauhukumu kuwa mkosa. Huu ndio urithi
wa watumishi wa Bwana, na haki yao inayotoka kwangu mimi, asema Bwana.”
Ayubu 42:1-2 “Ndipo Ayubu akamjibu Bwana,
na kusema. Najua ya kuwa waweza kufanya mambo yote, Na ya kuwa makusudi yako
hayawezi kuzuilika.”
Adui zako watakapojaribu
kukushambulia na hatimaye watagundua kuwa hauwezekaniki na kuwa mkono wa Bwana
uko juu yako watakuogopa kwa sababu watabaini ya kuwa Bwana Mungu wako yuko
pamoja nawe
1Samuel 18:12-16 “Sauli akamwogopa Daudi,
kwa sababu Bwana alikuwa pamoja naye, ila amemwacha Sauli. Kwa ajili ya hayo
Sauli akamwondosha kwake, akamfanya awe akida wake juu ya askari elfu; naye
akatoka na kuingia mbele ya watu. Naye Daudi akatenda kwa busara katika njia
zake zote naye Bwana alikuwa pamoja naye. Sauli alipoona ya kwamba alitenda kwa
busara sana, yeye alimwogopa. Lakini Israeli wote na Yuda wakampenda Daudi; kwa
kuwa alitoka na kuingia mbele yao.”
Kusudi la Mungu haliwezi kufutwa na wivu wa wanadamu
Ni muhimu kufahamu kuwa kusudi la
Mungu ndani yako haliwezi kufutwa na wivu wa wanadamu, Farao alipanga njama za
kila aina kujaribu kuwaangamiza Israel lakini kila alichokikusudia kilikuwa
kinyume na hakikuweza kufanikiwa hii ni kwa sababu Mungu alikuwa pamoja nao,
Mungu akiwa upande wako hakuna mtawala mwenye nguvu, wala mwenye mamlaka wala
mwenye kijicheo chochote cha Dunia hii atakayeweza kuuzuia mpango Mungu dhidi
yako, walimuuza Yusufu na bado akawa mtawala, walimfukuza Daudi na bado akawa
mfalme, walimtupa Daniel shimoni lakini akatukuzwa, walimuua Yesu lakini
alifufuka siku ya tatu na kaburi halikuweza kumshika wewe kama mwana wa Mungu
na Mungu ana kusudi na wewe usiogope kwa sababu Mungu yuko na yu aweza
kukusaidia
Kutoka 1:8-12. “Basi akainuka mfalme mpya
kutawala Misri, asiyemjua Yusufu. Akawaambia watu wake, Angalieni, watu wa wana
wa Israeli ni wengi tena wana nguvu kuliko sisi.Haya! Na tuwatendee kwa akili,
wasije wakaongezeka; tena, ikitokea vita, wao nao wasije wakashikamana na adui
zetu na kupigana nasi, na kutoka katika nchi hii. Basi wakaweka wasimamizi juu
yao wawatese kwa mizigo yao. Nao wakamjengea Farao miji ya kuwekea akiba,
Pithomu na Ramesesi. Lakini kwa kadiri ya walivyowatesa ndivyo walivyoongezeka
na kuzidi kuenea. Nao walichukiwa kwa sababu ya wana wa Israeli.”
Kila mtu aliyeko katika nafasi
yoyote hapa duniani anapaswa kukumbuka kuwa Mungu ndiye anayetawala hatupaswi
kuwa na kiburi na majivuno au kutumia nafasi tulizo nazo kwaajili ya
kuwakandamiza wengine, Farao alijifikiri kuwa yeye ndiye mwenye mamlaka na kwa
sababu hiyo aliyatumia vibaya dhidi ya Israel, Mungu alikuja kumfutilia mbali
katika bahari ya Shamu na historia yake imeandikwa lakini yeye na majeshi yake
walifutika, Mungu hataaachilia watu wake waonelewe kamwe na kama mtu anatafuta
kupotea aendelee kucheza na watu wanaomtegemea Bwana!
Zaburi 105:14-15 “Hakumwacha mtu awaonee,
Hata wafalme aliwakemea kwa ajili yao. Akisema, Msiwaguse masihi wangu, Wala
msiwadhuru nabii zangu.”
Kama unamtegemea Mungu na
umemfanya Mungu kuwa kimbilio lako, umemfanya bwana kuwa ngao yako, Basi elewa
na kukumbuka ya kuwa, hakuna uchawi, wala fitina, wala chuki, wala mateso, wala
njama zinazoweza kumuangamiza mtu wa Mungu, au mtu ambaye Mungu ameweka mkono
wake, changamoto na mateso tunayoyapitia hayamaanishi kuwa Mungu amewatupa watu
wake, Neno la Mungu linaonyesha wazi kuwa Israel walikuwa katika mapenzi ya
Mungu lakini walionelewa tu na Mungu alikuja kuingilia kati kwaajili ya utukufu
wake, usiwagope wanaokunyanyasa kwa sababu historia yao itafutika upesi,
changamoto unazozipitia haziwezi kamwe kufuta mpango wa Mungu, na kwa bahati
mbaya sasa kadiri wanavyokutesa ndivyo unavyozidi kuongezeka ila wao hawajui, Farao
alipopanga kuwapunguza Mungu alipanga kuwaongeza, Farao alipokusudia
kuwadhoofisha Mungu alikusudia kuwatia nguvu, Farao alipodhani kuwa atawamaliza
Mungu alikuwa anakusudia kuutimiza mpango wake kwa msingi huo kama unapitia
dhiki yoyote ile leo usiogope ni njia ya Mungu ya kukuongeza katika ulimwengu
wa roho, kupigana na mtu ambaye Mungu ameweka mkono wake au kumtesa au
kumzushia, au kufanya hila na njama
zozote hakuwezi kumfanya Mungu mwenye haki asimtokee Kadiri walivyowatesa
ndivyo walivyoongezeka!
Na. Rev. Innocent Samuel Kamote
Mkuu wa wajenzi mwenye Hekima

.jpg)

