Jumapili, 2 Agosti 2026

Wito wa kumtumikia Mungu katika huduma!


Matendo 13:1-3 “Na huko Antiokia katika kanisa lililokuwako palikuwa na manabii na waalimu, nao ni Barnaba, na Simeoni aitwaye Nigeri, na Lukio Mkirene, na Manaeni aliyekuwa ndugu wa kunyonya wa mfalme Herode, na Sauli. Basi hawa walipokuwa wakimfanyia Bwana ibada na kufunga, Roho Mtakatifu akasema, Nitengeeni Barnaba na Sauli kwa kazi ile niliyowaitia. Ndipo wakiisha kufunga na kuomba, wakaweka mikono yao juu yao, wakawaacha waende zao.”



Utangulizi:

Ni muhimu kufahamu kuwa Mungu anatoa wito kwa watu wake wote kuhakikisha ya kuwa wanamtumikia, Neno wito linamaanisha kualikwa na Mungu ili tuweze kutekeleza ajenda zake au kusudi lake ambalo amelikusudia yeye mwenyewe sawasawa na maagizo yaliyomo katika neno lake, Mungu huchagua watu wake wale anaowataka mwenyewe na kuwaalika wawe na ushirika naye na kisha awatume katika kazi yake ili kutekeleza mapenzi yake, kusudi lake na kazi yake hapa duniani na kwa sababu hiyo kuitikia wito wa kumtumikia Mungu ni utii usio na mashart

Marko 3:13-15 “Akapanda mlimani, akawaita aliowataka mwenyewe; wakamwendea. Akaweka watu kumi na wawili, wapate kuwa pamoja naye, na kwamba awatume kuhubiri, tena wawe na amri ya kutoa pepo.”

Kwa hiyo tangu nyakati za agano la kale Mungu amekuwa na tabia ya kuwaita na kuwachagua watu aliowataka mwenyewe kwaajili ya kutekeleza majukumu na makusudi yake yeye mwenyewe duniani, Kwa msingi huo kila mtu aliyeokoka anapaswa kuwa makini kumtumikia Mungu na kusikiliza sauti ya Mungu ili kutambua mapenzi ya Mungu katika maisha yake na kuwajibika mara moja katika kazi hii yenye Baraka na heshima kubwa, kwa bahati mbaya watu wengi sana hawapendi kumtumikia Mungu katika huduma mbalimbali Kanisani kwa kisingizio kuwa hawajaitwa, au kwa kutokuwa na ufahamu wanawajibika vipi, kwa hiyo leo tutachukua Muda kujifunza na kutafakari kwa pamoja somo hili muhimu kuhusu wito wa kumtumikia Mungu katika huduma kwa kuzingatia vipengele vikuu vitatu vifuatavyo:-


·         Maana ya neno wito katika maandiko.

·         Aina kuu tatu za wito katika huduma.

·         Jinsi Mungu anavyoita watu katika huduma.


Maana ya neno wito katika maandiko.

Ni muhimu kufahamu kuwa neno wito katika maandiko lina tajwa kwa lugha ya Kiebrania kwa neno “qara” na linatajwa kwa kiyunani kama neno “Kaleō” au “klēsis” ikimaanisha kuitwa, kutengwa, kuchaguliwa au kuteuliwa na Mungu kwa kusudi la kutimiza majukumu maalumu katika ajenda za Mungu, Kwa sababu hiyo wito sio mpango wala wazo la kibinadamu au shauku binafsi bali ni mpango kamili wa Mungu juu ya maisha ya mtu katika kusudi lake au kwa kazi maalumu, kwa hiyo wito katika huduma ni mualiko wa kumtumikia Mungu au kufanya kazi pamoja na Mungu katika kutimiza kusudi lake au ajenda zake mwenyewe hapa duniani kwa wakati maalumu.

Luka 5:27-29 “Baada ya hayo akatoka, akaona mtoza ushuru, jina lake Lawi, ameketi forodhani, akamwambia, Nifuate. Akaacha vyote, akaondoka, akamfuata. Na Lawi akamfanyia karamu kubwa nyumbani mwake; palikuwa na mkutano mkuu wa watoza ushuru na watu wengineo waliokuwa wameketi chakulani pamoja nao.”

Msingi mkuu wa Mungu anapomuita mtu kwanza anataka ushirika wa karibu na mtu huyo kisha ndipo amtume, kwa hiyo mtu aliyeitwa na aliyeitikia wito wa kumtumikia Mungu katika huduma anapaswa kuwa mtu mwenye ushirika wa karibu na Mungu, ushirika huu ni wa muhimu hata kabla ya kazi yenyewe

Yohana 21:15-17 “Basi walipokwisha kula, Yesu akamwambia Simoni Petro, Je! Simoni wa Yohana, wewe wanipenda kuliko hawa? Akamwambia, Naam, Bwana, wewe wajua kuwa nakupenda. Akamwambia, Lisha wana-kondoo wangu. Akamwambia tena mara ya pili, Simoni wa Yohana, wanipenda? Akamwambia, Ndiyo, Bwana, wewe wajua kuwa nakupenda. Akamwambia, Chunga kondoo zangu. Akamwambia mara ya tatu, Simoni wa Yohana, wanipenda? Petro alihuzunika kwa vile alivyomwambia mara ya tatu, Wanipenda? Akamwambia, Bwana, wewe wajua yote; wewe umetambua ya kuwa nakupenda. Yesu akamwambia, Lisha kondoo zangu.”

Marko 3:13-15 “Akapanda mlimani, akawaita aliowataka mwenyewe; wakamwendea. Akaweka watu kumi na wawili, wapate kuwa pamoja naye, na kwamba awatume kuhubiri, tena wawe na amri ya kutoa pepo.”

Kabla Mungu hajamuita mtu anataka ushirika na wewe anataka upendo wako na anataka uwe pamoja naye kisha ndipo akutume kuhubiri na kutoa pepo au kufanya huduma nyinginezo kwa niaba yake            

Aina kuu tatu za wito katika huduma.

Maandiko matakatifu yanaonyesha kuwa Mungu aliwaita watu kwa namna mbalimbali na kwaajili ya shughuli mbalimbali, kwa hiyo tunapozungumzia swala la wito tunazungumzia mada pana sana katika nyanja zote za kisiasa, kijamii na kiimani, na kisayansi, ukichunguza kwa kina utaweza kuona kuwa kote huko Mungu hufanya kazi ya kuwaita watu kwaajili ya makusudi mbalimbali, kwa hiyo wito hauko katika kuta za kanisa pekee unavuka mipaka na kwenda mbali zaidi ya vile tunavyofikiri, hata hivyo katika somo hili nataka kuzungumzia wito ambao unaishia ndani ya mipaka ya Kanisa pekee aina hizi za wito naweza kugawa katika makundi makuu muhimu matatu yafuatayo:-

·         Wito wa jumla katika wokovu

·         Wito wa jumla katika huduma

·         Wito maalumu katika huduma

Wito wa jumla katika wokovu – Wito huu wa ujumla katika wokovu ni wito unaotolewa na Mungu Roho Mtakatifu kwa jamii ya watu wote duniani ili wamuamini Bwana wetu Yesu Kristo kama mwokozi wao na kupokea uzima wa milele, huu ni wito unaotolewa kwa watu wote wamgeukie Mungu wamrudie yeye wamche yeye na kuwa na ushirika na yeye kwa hiyo watu wote duniani wanaalikwa kila iitwapo leo kupokea wito huu wa wokovu kwa imani.

Yohana 3:16-18 “Kwa maana jinsi hii Mungu aliupenda ulimwengu, hata akamtoa Mwanawe pekee, ili kila mtu amwaminiye asipotee, bali awe na uzima wa milele. Maana Mungu hakumtuma Mwana ulimwenguni ili auhukumu ulimwengu, bali ulimwengu uokolewe katika yeye. Amwaminiye yeye hahukumiwi; asiyeamini amekwisha kuhukumiwa; kwa sababu hakuliamini jina la Mwana pekee wa Mungu.”

Mathayo 11:28-30 “Njoni kwangu, ninyi nyote msumbukao na wenye kulemewa na mizigo, nami nitawapumzisha. Jitieni nira yangu, mjifunze kwangu; kwa kuwa mimi ni mpole na mnyenyekevu wa moyo; nanyi mtapata raha nafsini mwenu; kwa maana nira yangu ni laini, na mzigo wangu ni mwepesi.”

Warumi 8:28-30 “Nasi twajua ya kuwa katika mambo yote Mungu hufanya kazi pamoja na wale wampendao katika kuwapatia mema, yaani, wale walioitwa kwa kusudi lake. Maana wale aliowajua tangu asili, aliwachagua tangu asili wafananishwe na mfano wa Mwana wake, ili yeye awe mzaliwa wa kwanza miongoni mwa ndugu wengi. Na wale aliowachagua tangu asili, hao akawaita; na wale aliowaita, hao akawahesabia haki; na wale aliowahesabia haki, hao akawatukuza.”

Wito katika wokovu ni mwaliko wa jumla kwa jamii ya watu wote duniani wa kila kabila, na kila taifa na kila tamaduni na lugha na imani, wote wanapewa mwaliko wa kumpokea Yesu Kama Bwana na mwokozi wa maisha yao baada ya kuisikia injili na kuiamini na wote wanaopokea mwito huu kwa hiyari yao bila kulazimishwa wanafanyika kuwa watoto wa Mungu

Yohana 1:12-13 “Bali wote waliompokea aliwapa uwezo wa kufanyika watoto wa Mungu, ndio wale waliaminio jina lake; waliozaliwa, si kwa damu, wala si kwa mapenzi ya mwili, wala si kwa mapenzi ya mtu, bali kwa Mungu.”

Wito huu pamoja na mambo mengine pia unajumuisha kuishi maisha matakatifu na kuwa na ushirika na Mungu kumfanania Yesu Kristo na kuwa na tabia au mwenendo mwema kama yeye aliyetuita alivyo kwa hiyo kila aliyeokoka anawajibu wa kuukulia wokovu, kukomaa na kuwa kama Yesu Kristo mwenyewe alivyokua, wito huu ni wa toba, ni wito wa utakatifu, ni wito wa kupumzishwa na kusamehewa dhambi na kurudishwa katika familia ya Mungu na kuwa na uhusiano naye na kumuabudu

1Petro 1:14-16 “Kama watoto wa kutii msijifananishe na tamaa zenu za kwanza za ujinga wenu; bali kama yeye aliyewaita alivyo mtakatifu, ninyi nanyi iweni watakatifu katika mwenendo wenu wote; kwa maana imeandikwa, Mtakuwa watakatifu kwa kuwa mimi ni mtakatifu.”

Wito wa jumla katika huduma.

Wakati msingi wa wito wa kwanza ni kutengeneza mahusiano yetu na Mungu, mojawapo ya majukumu yetu vile vile ni kumtumikia Mungu, kila mtu aliyeokoka ameitwa kumtumikia Mungu kwa hivyo wote tuliookolewa pia tuna wajibu wa kumtumikia Mungu katika majukumu mbalimbali katika mwili wa Kristo, wito huu ni wito wa jumla kwa watu waliookoka unaowekwa na Roho Mtakatifu ndani yetu na kutubebesha majukumu ya jumla katika kuonyesha upendo kwa wengine, kumtii Mungu, kumuabudu na kuwashirikisha wengine imani yetu, wito huu unamuhusu kila mtu katika kanisa na sio viongozi au wachungaji peke yao wito huu unaonekana tangu nyakati za agano la kale.

Kumbukumbu 10:12-13 “Na sasa, Israeli, Bwana, Mungu wako, anataka nini kwako, ila umche Bwana, Mungu wako, na kwenda katika njia zake zote, na kumpenda, na kumtumikia Bwana, Mungu wako, kwa moyo wako wote, na kwa roho yako yote; kuzishika amri za Bwana na sheria zake, ninazokuamuru leo, upate uheri?

Zaburi 100:1-3 “Mfanyieni Bwana shangwe, dunia yote; Mtumikieni Bwana kwa furaha; Njoni mbele zake kwa kuimba; Jueni kwamba Bwana ndiye Mungu; Ndiye aliyetuumba na sisi tu watu wake; Tu watu wake, na kondoo wa malisho yake.”

Warumi 12:6-11 “Basi kwa kuwa tuna karama zilizo mbalimbali, kwa kadiri ya neema mliyopewa; ikiwa unabii, tutoe unabii kwa kadiri ya imani; ikiwa huduma, tuwemo katika huduma yetu; mwenye kufundisha, katika kufundisha kwake; mwenye kuonya, katika kuonya kwake; mwenye kukirimu, kwa moyo mweupe; mwenye kusimamia kwa bidii mwenye kurehemu, kwa furaha. Pendo na lisiwe na unafiki lichukieni lililo ovu, mkiambatana na lililo jema. Kwa pendo la udugu, mpendane ninyi kwa ninyi; kwa heshima mkiwatanguliza wenzenu; kwa bidii, si walegevu; mkiwa na juhudi katika roho zenu; mkimtumikia Bwana;”

Mathayo 28:18-20 “Yesu akaja kwao, akasema nao, akawaambia, Nimepewa mamlaka yote mbinguni na duniani. Basi, enendeni, mkawafanye mataifa yote kuwa wanafunzi, mkiwabatiza kwa jina la Baba, na Mwana, na Roho Mtakatifu; na kuwafundisha kuyashika yote niliyowaamuru ninyi; na tazama, mimi nipo pamoja nanyi siku zote, hata ukamilifu wa dahari.”

Unaona maandiko yana maagizo mengi ambapo kila mtu aliyeokolewa amepewa wajibu na anaagizwa kutumika, kila mtu aliyeokoka anaagizwa kuihubiri injili, anaagizwa kuomba anaagizwa kutoa anaagizwa kuwatumikia wengine anaagizwa kufungua na kupanda makanisa anaagizwa kufanya huduma zote, pamoja na mambo mengine tofauti ni kuwa watu hawa waliookolewa walioitwa katika wito wa ujumla watafanya kazi zao za kawaida huku wakifanya kazi za huduma kwa mujibu wa ratiba za maisha yao, na ratiba za kikanisa za kutumika kila iitwapo leo, aina hii ya wito ni wito wa ujumla katika wokovu ambapo waamini wanaagizwa kutumia vipawa vyao kumtumikia Mungu kwa  kadiri ya neema, wito huu unajumuisha kumuwakilisha Mungu popote tulipo pia iwe ni nyumbani au kazini au shuleni wewe ni wakili wa Yesu Kristo na unatumika pale ulipo kama chumvi na kama nuru.

Wito maalumu katika huduma

Wito huu au aina hii ya wito hutolewa kwa uwezo wa Roho Myakatifu kwa waamini kumuwezesha mtu huyo kusikia sauti ya Mungu kwa njia mbalimbali na kuamua kucha kila kitu hata kazi kwa kusudi la kumtumikia Mungu moja kwa moja katika kazi yake akiwa na huduma ya aidha mtume, au nabii, au mwinjilisti au mchungaji na au mwalimu aina hii pia ya huduma huwa inaambatana na huduma za kimaongozi katika kanisa na wakati mwingine karama mbalimbali za Roho Mtakatifu kuwawezesha watu hao kuuhudumia mwili wa Kristo kwa kuujenga na kuukamilisha

Waefeso 4:11-13 “Naye alitoa wengine kuwa mitume, na wengine kuwa manabii; na wengine kuwa wainjilisti na wengine kuwa wachungaji na waalimu; kwa kusudi la kuwakamilisha watakatifu, hata kazi ya huduma itendeke, hata mwili wa Kristo ujengwe; hata na sisi sote tutakapoufikia umoja wa imani na kumfahamu sana Mwana wa Mungu, hata kuwa mtu mkamilifu, hata kufika kwenye cheo cha kimo cha utimilifu wa Kristo;”

Jinsi Mungu anavyoita watu katika huduma.

Linapokuja swala la wito maalumu katika huduma watu wengi sana huwa wanajiuliza nitajuaje kama nina wito, tunapojifunza kipengele hiki kinachozungumzia jinsi Mungu anavyoita watu katika huduma tutapata ufahamu namna na jinsi Mungu anavyosema nasi kuhususiana na wito wetu kujifunza kuhusu swala hili kutatusaidia kutembea kwa uhakika katika huduma tukiwa na uhakika kuwa hatukubahatisha katika swala zima la kumtumikia Mungu katika kazi hii maalumu, Neno la Mungu linaainisha njia mbalimbali ambazo Mungu alizitumia kuwaita watu wake katika wito maalumu

1.       Mungu anaweza kumuita mtu kwa sauti yake moja kwa moja  - wakati mwingine Mungu huwaita watumishi wake moja kwa moja kwa sauti yake katika mifumo anayoijua yeye mwenyewe  watumishi wa Mungu kama Musa, Samuel na Paulo waliitwa moja kwa moja katika huduma kwa kuisikia sauti ya Bwana  wazi wazi moja ona

 

Kutoka 3:1-10 “Basi huyo Musa alikuwa akilichunga kundi la Yethro mkwewe, kuhani wa Midiani; akaliongoza kundi nyuma ya jangwa, akafika mpaka mlima wa Mungu, hata Horebu. Malaika wa BWANA akamtokea, katika mwali wa moto uliotoka katikati ya kijiti; akatazama, na kumbe! Kile kijiti kiliwaka moto, nacho kijiti hakikuteketea. Musa akasema, Nitageuka sasa, niyaone maono haya makubwa, na sababu kijiti hiki hakiteketei. BWANA alipoona ya kuwa amegeuka ili atazame, Mungu akamwita kutoka katikati ya kile kijiti, akasema, Musa! Musa! Akasema, Mimi hapa. Naye akasema, Usikaribie hapa; vua viatu vyako miguuni mwako; maana mahali hapo unaposimama ni nchi takatifu. Tena akasema, Mimi ni Mungu wa baba yako, Mungu wa Ibrahimu, Mungu wa Isaka, na Mungu wa Yakobo. Musa akaficha uso wake; kwa maana aliogopa kumwangalia Mungu. BWANA akasema, Hakika nimeyaona mateso ya watu wangu walioko Misri, nami nimekisikia kilio chao kwa sababu ya wasimamizi wao; maana nayajua maumivu yao; nami nimeshuka ili niwaokoe na mikono ya Wamisri, niwapandishe kutoka nchi ile, hata nchi njema, kisha pana; nchi ijaayo maziwa na asali; hata mahali pa Mkanaani, na Mhiti, na Mwamori, na Mperizi, na Mhivi, na Myebusi. Basi, tazama, kilio cha wana wa Israeli kimenifikilia; tena nimeyaona hayo mateso ambayo Wamisri wanawatesa. Haya, basi, nitakutuma sasa kwa Farao, ili upate kuwatoa watu wangu, hao wana wa Israeli, katika Misri.”

 

1Samuel 3:1-10 “Basi, mtoto Samweli akamtumikia Bwana mbele ya Eli. Na neno la Bwana lilikuwa adimu siku zile; hapakuwa na mafunuo dhahiri. Ikawa wakati huo, Eli alipokuwa amelala mahali pake (tena macho yake yalikuwa yameanza kupofuka, hata asiweze kuona), na taa ya Mungu ilikuwa haijazimika bado, na Samweli alikuwa amelala katika hekalu la Bwana, palipokuwa na sanduku la Mungu; basi, wakati huo Bwana akamwita Samweli; naye akasema, Mimi hapa. Akamwendea Eli kwa haraka, akasema, Mimi hapa; kwa maana uliniita. Akasema, Sikukuita; kalale tena. Naye akaenda, akalala tena.Bwana akaita mara ya pili, Samweli! Samweli! Akaondoka akamwendea Eli, akasema, Mimi hapa; kwa maana uliniita. Akajibu, Sikukuita, mwanangu; kalale tena. Basi Samweli alikuwa hamjui Bwana bado, na neno la Bwana lilikuwa bado halijafunuliwa kwake. Bwana akamwita Samweli mara ya tatu. Naye akaondoka akamwendea Eli, akasema, Mimi hapa; kwa maana uliniita. Ndipo Eli akatambua ya kuwa Bwana ndiye aliyemwita yule mtoto. Kwa hivyo Eli akamwambia Samweli, Enenda, kalale; itakuwa, akikuita, utasema, Nena, Bwana; kwa kuwa mtumishi wako anasikia. Basi Samweli akaenda akalala mahali pake. Bwana akaja, akasimama, akaita vile vile kama kwanza, Samweli! Samweli! Ndipo Samweli akasema, Nena, Bwana; kwa kuwa mtumishi wako anasikia.”

 

Matendo 9:1-6 “Lakini Sauli, akizidi kutisha na kuwaza kuwaua wanafunzi wa Bwana, akamwendea Kuhani Mkuu, akataka ampe barua za kuenda Dameski zilizoandikwa kwa masinagogi, ili akiona watu wa Njia hii, waume kwa wake, awafunge na kuwaleta Yerusalemu. Hata alipokuwa akisafiri, ikawa anakaribia Dameski; ghafula ikamwangaza kote kote nuru kutoka mbinguni. Akaanguka chini, akasikia sauti ikimwambia, Sauli, Sauli, mbona waniudhi? Akasema, U nani wewe, Bwana? Naye akasema, Mimi ndimi Yesu unayeniudhi wewe. Lakini simama, uingie mjini, nawe utaambiwa yakupasayo kutenda.”

 

2.       Mungu anaweza kuita watumishi wake kupitia maono – Maandiko yanaonyesha kuwa kwa njia ya maono pia Mungu anaweza kumuita mtu katika kazi yake maalumu na ikawa na ufanisi mkubwa, Nabii Isaya alipokea wito wake kupitia Maono na Mungu alimtumia kwa kiwango kikubwa sana  

 

Isaya 6:1-10. “Katika mwaka ule aliokufa mfalme Uzia nalimwona Bwana ameketi katika kiti cha enzi, kilicho juu sana na kuinuliwa sana, na pindo za vazi lake zikalijaza hekalu. Juu yake walisimama maserafi; kila mmoja alikuwa na mabawa sita; kwa mawili alifunika uso wake, na kwa mawili alifunika miguu yake, na kwa mawili aliruka. Wakaitana, kila mmoja na mwenzake, wakisema, Mtakatifu, Mtakatifu, Mtakatifu, ni Bwana wa majeshi; dunia yote imejaa utukufu wake. Na misingi ya vizingiti ikatikisika kwa sababu ya sauti yake aliyelia, nayo nyumba ikajaa moshi. Ndipo niliposema, Ole wangu! Kwa maana nimepotea; kwa sababu mimi ni mtu mwenye midomo michafu, nami ninakaa kati ya watu wenye midomo michafu; na macho yangu yamemwona Mfalme, Bwana wa majeshi.Kisha mmoja wa maserafi wale akaruka akanikaribia; naye alikuwa na kaa la moto mkononi mwake, ambalo alikuwa amelitwaa kwa makoleo toka juu ya madhabahu; akanigusa kinywa changu kwa kaa hilo, akaniambia, Tazama, hili limekugusa midomo yako, na uovu wako umeondolewa, na dhambi yako imefunikwa. Kisha nikaisikia sauti ya Bwana, akisema, Nimtume nani, naye ni nani atakayekwenda kwa ajili yetu? Ndipo niliposema, Mimi hapa, nitume mimi. Naye akaniambia, Enenda, ukawaambie watu hawa, Fulizeni kusikia, lakini msifahamu; fulizeni kutazama, lakini msione. Uunoneshe moyo wa watu hawa, ukayatie uzito masikio yao, ukayafumbe macho yao; wasije wakaona kwa macho yao, na kusikia kwa masikio yao, na kufahamu kwa mioyo yao, na kurejea na kuponywa.

 

3.       Mungu anaweza kuita watumishi wake kupitia ndoto – Mungu hutumia ndoto pia kufunua kusudu lake, mpango wake na agenda zake wito maalumu wa Yusufu ulifunuliwa kupitia ndoto mapema sana katika maisha yake tangu akiwa mdogo kuwa Mungu angemtumia, kupitia hili tunaweza kujifunza hapa na kutambua ya kuwa Mungu ameita baadhi ya watu wake kumtumikia kwa kutumia njia anazoona kuwa inafaa ikiwa ni pamoja na ndoto, Mungu anatumia njia ambayo muhusika ataelewa kwa urahisi au njia hiyo inaeleweka kwa mtu huyo.

 

Mwanzo 37:5-11 “Yusufu akaota ndoto, akawapa ndugu zake habari, nao wakazidi kumchukia; akawaambia, Tafadhalini, sikieni ndoto hii niliyoiota. Tazama, sisi tulikuwa tukifunga miganda shambani, kumbe! Mganda wangu ukaondoka ukasimama, na tazama, miganda yenu ikazunguka ikainama mbele ya mganda wangu. Ndugu zake wakamwambia, Je! Kweli wewe utatumiliki sisi? Nawe utatutawala sisi? Wakazidi kumchukia kwa ajili ya ndoto yake, na kwa maneno yake. Akaota tena ndoto nyingine, akawaambia ndugu zake, akasema, Angalieni, nimeota ndoto nyingine; na tazama, jua na mwezi na nyota kumi na moja zikaniinamia. Akawaambia baba yake na ndugu zake; baba yake akamkemea akamwambia, Ni ndoto gani hii uliyoiota? Je! Mimi na mama yako na ndugu zako tutakuja tukusujudie hata nchi? Ndugu zake wakamhusudu; bali baba yake akalihifadhi neno hili.”

 

4.       Mungu huweza kuita watumishi wake kupitia mtumishi wake au nabii – Wako watu kadhaa katika maandiko ambao waliitwa katika kazi maalumu kupitia manabii, Nabii alifunuliwa na kumtia mafuta yule aliyekusudiwa katika wito fulani, kwa mfano ufalme wa Sauli, au ufalme wa Daudi,  au  nabii Elisha hawa waliitwa kupitia nabii au mtumishi wa Mungu aliyekuwako wakati huo, wao kupitia ujuzi na sauti ya Roho Mtakatifu wanaweza kumjua na kumbaini mtu ambaye Mungu amemuita katika huduma  na akafaa kwaajili ya utumishi huo uliokusudiwa!

 

1Samuel 9:15-20 “Basi Bwana alikuwa amemfunulia Samweli, siku moja kabla Sauli hajamwendea, akisema, Kesho, wakati kama huu, nitakuletea mtu kutoka nchi ya Benyamini, nawe mtie mafuta ili awe mkuu juu ya watu wangu Israeli, naye atawaokoa watu wangu na mikono ya Wafilisti; maana nimewaangalia watu wangu, kwa sababu kilio chao kimenifikilia. Hata Samweli alipomwona Sauli, Bwana akamwambia, Huyu ndiye niliyekuambia habari zake; huyu ndiye atakayewamiliki watu wangu. Ndipo Sauli akamkaribia Samweli langoni, akasema, Tafadhali, uniambie, nyumba ya mwonaji iko wapi? Samweli akamjibu Sauli, akasema, Mimi ndimi mwonaji; tangulia mbele yangu ukwee mpaka mahali pa juu, kwa maana mtakula pamoja nami leo; kisha, asubuhi nitakuacha uende zako, nami nitakuambia yote uliyo nayo moyoni mwako. Na wale punda zako waliopotea siku hizi tatu, usijiudhi kwa ajili yao; maana wameonekana. Na yote yaliyotamanika katika Israeli amewekewa nani? Si wewe, na nyumba yote ya baba yako?

 

1Samuel 16:13 “Ndipo Samweli akaitwaa pembe yenye mafuta, akamtia mafuta kati ya ndugu zake; na roho ya Bwana ikamjilia Daudi kwa nguvu tangu siku ile. Basi Samweli akaondoka, akaenda zake Rama.”  

 

1Wafalme 19:19-21 “Basi, akaondoka huko, akamkuta Elisha mwana wa Shafati, aliyekuwa akilima, mwenye jozi za ng'ombe kumi na mbili mbele yake, na yeye mwenyewe alikuwa pamoja na lile la kumi na mbili. Eliya akapita karibu naye, akatupa vazi lake juu yake. Naye akawaacha ng'ombe, akamfuata Eliya mbio, akasema, Nipe ruhusa, nakuomba, nimbusu baba yangu na mama yangu, kisha mimi nitakufuata. Akamwambia, Enenda, urudi; ni nini niliyokutendea? Akarudi akiacha kumfuata, akatwaa lile jozi la ng'ombe, akawachinja, akatokosa nyama zao kwa ile miti ya ng'ombe, akawapa watu, wakala. Kisha akainuka, akamfuata Eliya, akamhudumia.”

 

5.       Mungu huweza kuwaita watumishi wake kupitia malaika – Wakati mwingine Mungu humtuma malaika wake kuweza kuwasilisha ujumbe wa jukumu lake kwa mtumishi wake anayekusudiwa, Katika maandikio iko mifano mingi lakini tutaangalia mifano michache ya watu kadhaa kama Gideoni na Mariam mama yake Yesu ambao walipewa kazi maalumu kwa ujumbe wa malaika

 

Waamuzi 6:11-14 “Malaika wa Bwana akaenda akaketi chini ya mwaloni uliokuwa katika Ofra, uliokuwa mali yake Yoashi, Mwabiezeri; na mwanawe Gideoni alikuwa akipepeta ngano ndani ya shinikizo, ili kuificha machoni pa Wamidiani. Malaika wa Bwana akamtokea, akamwambia, Bwana yu pamoja nawe, Ee shujaa. Gideoni akamwambia, Ee Bwana wangu, ikiwa Bwana yu pamoja nasi, mbona mambo haya yote yametupata? Yako wapi matendo yake ya ajabu, waliyotuhadithia baba zetu, wakisema, Je! Siye Bwana, aliyetuleta huku kutoka Misri? Ila sasa ametutupa, naye ametutia katika mikono ya Midiani. Bwana akamtazama, akasema, Enenda kwa uwezo wako huu, ukawaokoe Israeli na mkono wa Midiani. Je! Si mimi ninayekutuma? 

 

Luka 1:26-33 “Mwezi wa sita, malaika Gabrieli alitumwa na Mungu kwenda mpaka mji wa Galilaya, jina lake Nazareti, kwa mwanamwali bikira aliyekuwa ameposwa na mtu, jina lake Yusufu, wa mbari ya Daudi; na jina lake bikira huyo ni Mariamu. Akaingia nyumbani kwake akasema, Salamu, uliyepewa neema, Bwana yu pamoja nawe. Naye akafadhaika sana kwa ajili ya maneno yake, akawaza moyoni, Salamu hii ni ya namna gani? Malaika akamwambia, Usiogope, Mariamu, kwa maana umepata neema kwa Mungu. Tazama, utachukua mimba na kuzaa mtoto mwanamume; na jina lake utamwita Yesu. Huyo atakuwa mkuu, ataitwa Mwana wa Aliye juu, na Bwana Mungu atampa kiti cha enzi cha Daudi, baba yake. Ataimiliki nyumba ya Yakobo hata milele, na ufalme wake utakuwa hauna mwisho.”

 

6.       Mungu huweza kuwaita watumishi wake kupitia Roho wake Mtakatifu – Ikumbukwe kuwa njia zote hizo Roho Mtakatifu ambaye ndiye Bwana wa mavuno anazitumia katika kuhakikisha kuwa wanapatikana watenda kazi katika mashamba yake lakini hutokea wakati mwingine mwenyewe akazungumza moja kwa moja kwa njia ya unabii na kumuita au kumtaka mtu katika huduma maalumu

 

Matendo 13:1-3 “Na huko Antiokia katika kanisa lililokuwako palikuwa na manabii na waalimu, nao ni Barnaba, na Simeoni aitwaye Nigeri, na Lukio Mkirene, na Manaeni aliyekuwa ndugu wa kunyonya wa mfalme Herode, na Sauli. Basi hawa walipokuwa wakimfanyia Bwana ibada na kufunga, Roho Mtakatifu akasema, Nitengeeni Barnaba na Sauli kwa kazi ile niliyowaitia. Ndipo wakiisha kufunga na kuomba, wakaweka mikono yao juu yao, wakawaacha waende zao.”

 

7.       Mungu huweza kuwaita watumishi wake Kupitia Yesu Kristo mwenyewe – Wanafunzi wale kumi na wawili walikuwa ni chaguo la Yesu Kristo mwenyewe na aliwaita kama alivyopenda yeye mwenyewe hata sasa Yesu Kristo bado anaita watu wake kama apendavyo kwa njia mbalimbali na wakati mwingine yeye mwenyewe. Hata hivyo ni muhimu kuelewa kuwa katika njia hizo zote hakuna iliyobora zaidi kuliko nyingine kwa sababu zote ni njia ambazo yeye mwenyewe anazitumia kuwapata watu wa kumtumikia katika huduma maalumu, kwa hoyo mtumishi aliyetokewa na Yesu mwenyewe na kuitwa katika wito haimaanishi kuwa anaubora kushinda aliyeitwa kwa njia nyingine, kwani kimaandiko hizo zote ni nnia anazozitumia Mungu kufahamisha watu wake namna anavyowahitaji katika huduma.

 

Mathayo 4:18-19 “Naye alipokuwa akitembea kando ya bahari ya Galilaya, aliona ndugu wawili, Simoni aitwaye Petro, na Andrea nduguye, wakitupa jarife baharini; kwa maana walikuwa wavuvi. Akawaambia, Nifuateni, nami nitawafanya kuwa wavuvi wa watu.Mara wakaziacha nyavu zao, wakamfuata.”

 

Mathayo 9:9. “Naye Yesu alipokuwa akipita kutoka huko aliona mtu ameketi forodhani, aitwaye Mathayo, akamwambia, Nifuate. Akaondoka, akamfuata.”                                    

Kwa hiyo tunajifunza kuwa ni Mungu mwenyewe ndiye anayeita watu wake katika huduma, na kwa sababu hiyo hakuna mtu ajitwaliaye heshima hii, wakati Mungu anapomuita mtu kwaajili ya huduma mtu huyo huwekewa kitu cha ziada na neema ya juu zaidi ili aweze kuwahudumia wengine, Hata hivyo bado hatuwezi kuwaachia hao peke yao walioitwa katika wito maalumu wa huduma kwa sababu kazi ya Mungu ni pana na hivyo wale wote ambao hawatakuwa wameitwa katika wito maalumu wanabaki katika wito wa ujumla wa kumtumikia Mungu na wakifanya kwa uaminifu na utii kazi ya Mungu itasonga mbele na kuwa Baraka kubwa kwa jamii, Unaweza kujua wito wako kupitia neno la Mungu, kupitia maombi, kupitia shuhuda za huduma za watu unao wahudumia, kuthibitishwa na viongozi, na amani ya moyo, wito ni zawadi, wito ni heshima, wito ni kuaminiwa, wito ni wajibu na kwa sababu hiyo kama Mungu amekuweka katika ajenda zake basi wewe ni wa muhimu sana itikia sauti ya Mungu leo ukamtumikie.

Yohana 12:26 “Yeye aipendaye nafsi yake ataiangamiza; naye aichukiaye nafsi yake katika ulimwengu huu ataisalimisha hata uzima wa milele.Mtu akinitumikia, na anifuate; nami nilipo, ndipo na mtumishi wangu atakapokuwapo. Tena mtu akinitumikia, Baba atamheshimu.”

Waebrania 3:14-15 “Kwa maana tumekuwa washirika wa Kristo, kama tukishikamana na mwanzo wa uthabiti wetu kwa nguvu mpaka mwisho; hapo inenwapo, Leo, kama mtaisikia sauti yake, Msifanye migumu mioyo yenu, Kama wakati wa kukasirisha.”                    

Na Rev. Innocent Samuel Kamote

Mkuu wa wajenzi mwenye Hekima

Jumapili, 26 Julai 2026

UMUHIMU WA SHULE YA HUDUMA.


 

Waefeso 4:11-12 “Naye alitoa wengine kuwa mitume, na wengine kuwa manabii; na wengine kuwa wainjilisti na wengine kuwa wachungaji na waalimu; kwa kusudi la kuwakamilisha watakatifu, hata kazi ya huduma itendeke, hata mwili wa Kristo ujengwe;”



Utangulizi:

Ni muhimu kufahamu kuwa kusudi kubwa la shule ya huduma ndani ya kanisa ni kwaajili ya kukumbushana wajibu wetu wa kulijenga kanisa la Mungu, Mungu alitoa wengine kuwa Mitume, wengine kuwa Manabii, wengine kuwa Wainjilisti, wengine kuwa Wachungaji na Walimu kwa kusudi la kuwakamilisha watakatifu, na kuhakikisha kazi ya huduma inatendeka na mwili wa Kristo unajengwa kwa hiyo kila mtenda kazi ni mjenzi katika nyumba ya Mungu Kanisa la Mungu linafananishwa na shamba, linafananishwa na jengo na sisi ndio wafanyakazi pamoja na Mungu kwa hiyo kila mtenda kazi ni mjenzi katika nyumba ya Mungu na tunapaswa kuifanya kazi yetu vema na kwa usahihi kwa sababu Mungu ataipima kazi ya kila mtu kwa hiyo kila mjenzi anapaswa kuwa makini namna anavyojenga katika jengo la Mungu.

1Wakorintho 3:6-15 “Mimi nilipanda, Apolo akatia maji; bali mwenye kukuza ni Mungu. Hivyo, apandaye si kitu, wala atiaye maji, bali Mungu akuzaye. Basi yeye apandaye, na yeye atiaye maji ni wamoja, lakini kila mtu atapata thawabu yake mwenyewe sawasawa na taabu yake mwenyewe. Maana sisi tu wafanya kazi pamoja na Mungu; ninyi ni shamba la Mungu, ni jengo la Mungu. Kwa kadiri ya neema ya Mungu niliyopewa, mimi, kama mkuu wa wajenzi mwenye hekima, naliuweka msingi, na mtu mwingine anajenga juu yake. Lakini kila mtu na aangalie jinsi anavyojenga juu yake. Maana msingi mwingine hakuna mtu awezaye kuuweka, isipokuwa ni ule uliokwisha kuwekwa, yaani, Yesu Kristo. Lakini kama mtu akijenga juu ya msingi huo, dhahabu au fedha au mawe ya thamani, au miti au majani au manyasi, kazi ya kila mtu itakuwa dhahiri. Maana siku ile itaidhihirisha, kwa kuwa yafunuliwa katika moto; na ule moto wenyewe utaijaribu kazi ya kila mtu, ni ya namna gani. Kazi ya mtu aliyoijenga juu yake ikikaa, atapata thawabu. Kazi ya mtu ikiteketea, atapata hasara; ila yeye mwenyewe ataokolewa; lakini ni kama kwa moto.”

Katika nyumba ya Mungu kuna maeneo mbalimbali ambayo yanatutaka sisi kama watenda kazi kuwa makini, kuwa macho na kuyasimamia endapo tunataka kanisa letu likue kiroho na liwe kubwa lenye maelfu ya watu, ikumbukwe kuwa kadiri kanisa linavyokuwa kubwa linahitaji wahudumu wengi zaidi watakaotoa macho na kuhudumia maeneo mbalimbali na kumbuka kila tunapohudumu tunahudumia pamoja na Mungu kwa hiyo Baraka za Mungu huwa kubwa kwa kila mtenda kazi anayeifanya kazi yake kwa uaminifu, watenda kazi wengi wanapotupia macho maeneo mbalimbali ya kihuduma tunawapa watumishi wa Mungu nafasi kubwa ya kuomba na kulihudumia neno badala ya kushughulika na maswala ambayo yangeliweza kuangaliwa na watu wengine, aidha kanisa linapokua linatakiwa kuwa na wahudumu wengi zaidi ili kuzuia manung’unuiko miongoni mwa jumuiya ya  washirika katika kanisa la Mungu.

Matendo 6:1-4 “Hata siku zile wanafunzi walipokuwa wakiongezeka hesabu yao, palikuwa na manung'uniko ya Wayahudi wa Kiyunani juu ya Waebrania kwa sababu wajane wao walisahauliwa katika huduma ya kila siku. Wale Thenashara wakawaita jamii ya wanafunzi, wakasema, Haipendezi sisi kuliacha neno la Mungu na kuhudumu mezani. Basi ndugu, chagueni watu saba miongoni mwenu, walioshuhudiwa kuwa wema, wenye kujawa na Roho, na hekima, ili tuwaweke juu ya jambo hili; na sisi tutadumu katika kuomba na kulihudumia lile Neno.”

Kwa msingi huo basi tutachukua muda kujifunza somo hili UMUHIMU WA SHULE YA HUDUMA kwa kuzingatia vipengele vitatu vifuatavyo;-


  • Sisi tu wafanyakazi pamoja na Mungu
  • Jinsi tunavyoweza kujenga pamoja na Mungu
  • Vema mtumwa mwema na mwaminifu

 

Sisi tu wafanyakazi pamoja na Mungu.

Paulo mtume anaelezea wazi kuwa sisi tu wafanyakazi pamoja na Mungu, anasema hayo kwa kusudi la kuweka mkazo kuwa kazi ya Mungu haiwezi kwenda mbele bila wanadamu, Mungu alimuumba mwanadamu kwa kusudi la kuwa na ushirika na yeye na kwa sababu hiyo sisi tunabeba kusudi lote la Mungu hapa duniani, jukumu hili kamwe Mungu hajawahi kuwapa malaika lakini ametupa sisi, kwa hiyo ni jukumu la kila mtu aliyeokolewa kulijemga kanisa la Mungu na kuifanya kazi ya Mungu kazi hii iliyo njema.

1Wakorintho 3:9 “Maana sisi tu wafanya kazi pamoja na Mungu; ninyi ni shamba la Mungu, ni jengo la Mungu.”

2Wakorintho 6:1-2 “Nasi tukitenda kazi pamoja naye twawasihi msiipokee neema ya Mungu bure. (Kwa maana asema, Wakati uliokubalika nalikusikia, Siku ya wokovu nalikusaidia; tazama, wakati uliokubalika ndiyo sasa; tazama siku ya wokovu ni sasa)

Mungu amempa mwanadamu jukumu zima la kuihubiri injili na kuieneza na kuwafanya mataifa yote kuwa wanafunzi, hii ni heshima kubwa sana kwani tunapoifanya kazi hiii Mungu huwa hakuachi anakuwa pamoja nawe kwa sababu kazi hii sio yetu ni ya kwake kwa hiyo wewe kama mtoto wake unashirikiana naye katika kuikamilisha hakuna mahali popote ambapo Mungu alimuagiza mtu kazi kisha akamuacha, wakati wote mtu anapoifanya kazi ya Mungu neno la Mungu linaonyesha kuwa Bwana akawa pamoja naye

Marko 16:19-20. “Basi Bwana Yesu, baada ya kusema nao, akachukuliwa juu mbinguni, akaketi mkono wa kuume wa Mungu. Nao wale wakatoka, wakahubiri kotekote, Bwana akitenda kazi pamoja nao, na kulithibitisha lile neno kwa ishara zilizofuatana nalo.]

Paulo anatumia mfano wa shughuli za kilimo kama kupanda na kumwagilia na hata maswala ya ujenzi kuonyesha kuwa katika mwili wa Kristo kila mmoja wetu ana majukumu mbalimbali, kutokana na vipawa mbalimbali na karama mbalimbali  lakini wote sisi tunaifanya kazi moja, kwa hiyo katika shule hii ya watenda kazi tunaainisha maeneo mbalimbali ya kiutendaji , hata kama wote tunajifunza hizi ili kumtumikia Mungu kwa pamoja baadae utaweza kuona kuwa tutamtumikia Mungu sehemu mbalimbali na kufanya huduma mbalimbali lakini katika mwili huu huu mmoja.

1Wakorintho 12:12-27 “Maana kama vile mwili ni mmoja, nao una viungo vingi, na viungo vyote vya mwili ule, navyo ni vingi, ni mwili mmoja; vivyo hivyo na Kristo. Kwa maana katika Roho mmoja sisi sote tulibatizwa kuwa mwili mmoja, kwamba tu Wayahudi, au kwamba tu Wayunani; ikiwa tu watumwa au ikiwa tu huru; nasi sote tulinyweshwa Roho mmoja. Kwa maana mwili si kiungo kimoja, bali ni vingi. Mguu ukisema, Kwa kuwa mimi si mkono, mimi si wa mwili; je! Si wa mwili kwa sababu hiyo? Na sikio likisema, Kwa kuwa mimi si jicho, mimi si la mwili; je! Si la mwili kwa sababu hiyo? Kama mwili wote ukiwa jicho, ku wapi kusikia? Kama wote ni sikio ku wapi kunusa? Bali Mungu amevitia viungo kila kimoja katika mwili kama alivyotaka. Lakini kama vyote vingekuwa kiungo kimoja, mwili ungekuwa wapi? Lakini sasa viungo ni vingi, ila mwili ni mmoja. Na jicho haliwezi kuuambia mkono, Sina haja na wewe; wala tena kichwa hakiwezi kuiambia miguu, Sina haja na ninyi. Bali zaidi sana vile viungo vya mwili vidhaniwavyo kuwa vinyonge zaidi vyahitajiwa zaidi. Na vile viungo vya mwili vidhaniwavyo kuwa havina heshima, viungo vile twavipa heshima zaidi; na viungo vyetu visivyo na uzuri vina uzuri zaidi sana. Kwa maana viungo vyetu vilivyo na uzuri havina uhitaji; bali Mungu ameuungamanisha mwili, na kukipa heshima zaidi kile kiungo kilichopungukiwa;ili kusiwe na faraka katika mwili, bali viungo vitunzane kila kiungo na mwenziwe. Na kiungo kimoja kikiumia, viungo vyote huumia nacho, na kiungo kimoja kikitukuzwa, viungo vyote hufurahi pamoja nacho. Basi ninyi mmekuwa mwili wa Kristo, na viungo kila kimoja peke yake.”

Kwa hiyo tutafanya kazi katika maeneo tofauti tofauti wakati mwingine kwa kupangiwa au wakati mwingine kutokana na kile kitu ambacho Mungu amekiweka ndani yako lakini sisi sote tu watenda kazi na tufahamu kuwa tunaifanya kazi moja, asitokee mtenda kazi akafikiri kuwa hajaheshimiwa kwa kupangiwa eneo fulani, kokote tutakakoenda kumbuka Bwana yuko pamoja nawe na anajua kuwa unaujenga mwili wa Kristo, aidha tunafanya huduma hizi kwa neema ya Mungu kwa hiyo neema zinatofautiana kinachotakiwa kwetu ni uaminifu, usitake kuwa na huduma kama ya fulani kwa sababu kila mmoja ana neema tofauti na hivyo tutatumia neema hizo kwa kufaidiana

Waefeso 4:7-8 “Lakini kila mmoja wetu alipewa neema kwa kadiri ya kipimo cha kipawa chake Kristo. Hivyo husema, Alipopaa juu aliteka mateka, Akawapa wanadamu vipawa.”

1Petro 10-11 “kila mmoja kwa kadiri alivyoipokea karama, itumieni kwa kuhudumiana; kama mawakili wema wa neema mbalimbali za Mungu. Mtu akisema, na aseme kama mausia ya Mungu; mtu akihudumu, na ahudumu kwa nguvu anazojaliwa na Mungu; ili Mungu atukuzwe katika mambo yote kwa Yesu Kristo. Utukufu na uweza una yeye hata milele na milele. Amina.”

Warumi 12:3-5 “Kwa maana kwa neema niliyopewa namwambia kila mtu aliyeko kwenu asinie makuu kupita ilivyompasa kunia; bali awe na nia ya kiasi, kama Mungu alivyomgawia kila mtu kiasi cha imani. Kwa kuwa kama vile katika mwili mmoja tuna viungo vingi, wala viungo vyote havitendi kazi moja; Vivyo hivyo na sisi tulio wengi tu mwili mmoja katika Kristo, na viungo, kila mmoja kwa mwenzake.”               

Kwa hiyo utaweza kuona Mungu ametuita kutenda kazi pamoja naye kwa neema na vipawa na karama tofauti tofauti, tutumie kila alichotupa Mungu kumtumikia bila kuumiza mwili wa Kristo kwa migawanyiko na manung’uniko mbalimbali kwani wote tutaifanya kazi hii kwa kufikia lengo moja kuufikia ulimwengu na kuwaleta watu kwa Yesu na kulijenga kanisa lake ili baada ya utumishi wetu duniani tukakae naye kule mbinguni

Jinsi tunavyoweza kujenga pamoja na Mungu

Katika kanisa la Mungu kuna namna mbalimbali za utumishi ambazo kwazo tunaweza kuzitumia katika kumtumikia Mungu, Ni muhimu kwetu kufahamu kuwa tukiifanya kazi hii ya Mungu kwa hiyari, kwa moyo na kwa uaminifu Mungu mwenyewe atakupa thawabu na kukupongeza na kukufuta machozi kwa kazi hii ambayo ina upinzani kutoka kwa adui shetani lakini simama kwa uaminifu kwaajili ya Bwana kama alivyofanya mtume Paulo ambaye alivumilia

Mathayo 25:21-23. “Akaja yule aliyepokea talanta tano, akaleta talanta nyingine tano, akisema, Bwana, uliweka kwangu talanta tano; tazama, talanta nyingine tano nilizopata faida. Bwana wake akamwambia, Vema, mtumwa mwema na mwaminifu; ulikuwa mwaminifu kwa machache, nitakuweka juu ya mengi; ingia katika furaha ya bwana wako. Akaja na yule aliyepokea talanta mbili, akasema, Bwana, uliweka kwangu talanta mbili; tazama, talanta nyingine mbili nilizopata faida. Bwana wake akamwambia, Vema, mtumwa mwema na mwaminifu; ulikuwa mwaminifu kwa machache, nitakuweka juu ya mengi; ingia katika furaha ya bwana wako.”

Washirika wanapohudumiwa vema na kufikiwa katika mazingira yote hasa katika makanisa makubwa wanaona kuwa wanajaliwa hata kama hawamuoni mchungaji kiongozi kutokana na majukumu yake umoja wa kanisa utaimarika, kanisa letu litakuwa kwa kasi kwa ukuaji wa aina zote nazungumzia ukuaji wa kiroho, ukomavu na wa kiidadi na kuwa kanisa la maelfu, umoja utaimarika hata pamoja na ukubwa wa kanisa, na wingi wetu utageuka utajiri na afya ya kila mmoja wetu na miujiza haitakoma umati utavuta umati na Mungu atataka kujidhihirisha kwenye kusanyiko la watu wengi, sasa haya ndio maeneo na mazingira tunayoweza kumtumikia Mungu wetu:-

  1. Kuwahudumiwa waamini wapya – Mojawapo ya eneo Muhimu sana ambalo watenda kazi wote, wanafunzi wote na wenye hekima wote tunapaswa kulipa uzito mkubwa sana sana ili tupate kanisa lililobora ni kuwahudumia waamini wapya, au kuwahudumia watoto wachanga kiroho, kuwafuatilia, kuwalisha kwa neno la Mungu na kufanya malezi, Kama tunampenda sana Yesu upendo wetu utaonekana kwa jinsi tunavyowalisha kondoo zake

 

Yohana 21:15-17 “Basi walipokwisha kula, Yesu akamwambia Simoni Petro, Je! Simoni wa Yohana, wewe wanipenda kuliko hawa? Akamwambia, Naam, Bwana, wewe wajua kuwa nakupenda. Akamwambia, Lisha wana-kondoo wangu. Akamwambia tena mara ya pili, Simoni wa Yohana, wanipenda? Akamwambia, Ndiyo, Bwana, wewe wajua kuwa nakupenda. Akamwambia, Chunga kondoo zangu. Akamwambia mara ya tatu, Simoni wa Yohana, wanipenda? Petro alihuzunika kwa vile alivyomwambia mara ya tatu, Wanipenda? Akamwambia, Bwana, wewe wajua yote; wewe umetambua ya kuwa nakupenda. Yesu akamwambia, Lisha kondoo zangu.”

 

Agizo hili ni pana kwani linahusu ulishaji mzima wa kondoo, watumishi wa Mungu walioitwa katika wito maalumu wataifanya kazi ya kuwalisha kondoo katika ibada, tulizojipangia na katika semina zitakazojitokeza na kadhalika, lakini watenda kazi, wanafunzi na wenye hekima (Wiseman) wao watapaswa kuhakikisha kuwa wanawahudumia na kuwalisha watoto wachanga kiroho kwa kuwafundisha masomo ya mwanzo ya wokovu, ukiwaimarisha waamini wapya katika wokovu, kwa kuwaombea, kwa kuwafundisha kuisoma Biblia, na kuwaelekeza kuhusu maisha  tamaduni na Misingi  ya imani ya kanisa letu

 

  1. Kuwahudumia waamini wote ibadani    - Eneo lingine la huduma zetu kama watendakazi, wanafunzi na wenye hekima ni kuwahudumia watu wote wanaohudhuria ibada katika kanisa letu, watu waliopitia shule hii ya huduma watawahudumia watu kwa kuwapokea vizuri na kwa heshima, kuwapokelea vitu vyao, watoto na kuwaongoza mahali sahihi pa kuketi, sio hivyo tu kama ni mgeni utafanya kila jitihada kutambua anaitwa nani namba zake za simu na atakuwa pamoja nasi kwa muda gani, kama ni wadhaifu tutawatia nguvu, na tutaanza kuwapandisha imani kuwa umefanya uamuzi wa busara kuja kuabudu katika kanisa letu hili zuri, hakikisha kuwa kila mtu ana mazingira salama ya kuabudu, atajua vyoo viko wapi, wasaidie kujua mambo muhimu wanayopaswa kuyajua, tutakuwa tayari kuhudumu pamoja na Muhubiri katika ibada kuu na maombezi na kusawaidia watu wanaoanguka kwa mapepo au nguvu za Mungu na wale wanaofunguliwa na kuhakikisha kuwa tunawahifadhi kwa nguo maalumu safi na kuwafunika, Pia kuwapeleka mahali salama na sahihi zaidi na katika ibada nyingine maalumu kama ubatizo, meza ya Bwana, kubariki watoto, na kadhalika

 

Yohana 10:14 “Mimi ndimi mchungaji mwema; nao walio wangu nawajua; nao walio wangu wanijua mimi

 

1Wathesalonike 5:14 “Ndugu, twawasihi, waonyeni wale wasiokaa kwa utaratibu; watieni moyo walio dhaifu; watieni nguvu wanyonge; vumilieni na watu wote.”

 

Waefeso 4:1-3 “Kwa hiyo nawasihi, mimi niliye mfungwa katika Bwana, mwenende kama inavyoustahili wito wenu mlioitiwa; kwa unyenyekevu wote na upole, kwa uvumilivu, mkichukuliana katika upendo; na kujitahidi kuuhifadhi umoja wa Roho katika kifungo cha amani.”

 

  1. Kusaidia huduma ya kichungaji – Watendakazi wote, wanafunzi na wenye hekima wanapaswa pia kufanya kazi ya kutoa msaada wa huduma ya kichungaji, ikumbukwe kuwa Mchungaji hawezi kufanya kila kitu peke yake, na akilazimika kufanya yote muda wa kukaa katika neno la Mungu na maombi utafilisiwa na kuathiri huduma za kiroho za jumla  na ndio maana mitume waliona vema kuwa na mashemasi kwaajili ya majukumu

 

Matendo 6:1-7 “Hata siku zile wanafunzi walipokuwa wakiongezeka hesabu yao, palikuwa na manung'uniko ya Wayahudi wa Kiyunani juu ya Waebrania kwa sababu wajane wao walisahauliwa katika huduma ya kila siku. Wale Thenashara wakawaita jamii ya wanafunzi, wakasema, Haipendezi sisi kuliacha neno la Mungu na kuhudumu mezani. Basi ndugu, chagueni watu saba miongoni mwenu, walioshuhudiwa kuwa wema, wenye kujawa na Roho, na hekima, ili tuwaweke juu ya jambo hili; na sisi tutadumu katika kuomba na kulihudumia lile Neno. Neno hili likapendeza machoni pa mkutano wote; wakamchagua Stefano, mtu aliyejaa imani na Roho Mtakatifu, na Filipo, na Prokoro, na Nikanori, na Timoni, na Parmena, na Nikolao mwongofu wa Antiokia; ambao wakawaweka mbele ya mitume, na walipokwisha kuomba wakaweka mikono yao juu yao. Neno la Mungu likaenea; na hesabu ya wanafunzi ikazidi sana katika Yerusalemu; jamii kubwa ya makuhani wakaitii ile Imani.”

 

Warumi 16:3-4. “Nisalimieni Priska na Akila, watenda kazi pamoja nami katika Kristo Yesu; waliokuwa tayari hata kukatwa kichwa kwa ajili ya maisha yangu; ambao ninawashukuru, wala si mimi tu, ila na makanisa ya Mataifa yote pia; nisalimieni na kanisa lililomo katika nyumba yao.”

 

Kutoka 18:17-22 “Mkwewe Musa akamwambia, Jambo hili ufanyalo si jema. Huna budi utadhoofika wewe, na hawa watu walio pamoja nawe pia; maana jambo hili ni zito mno kwako; huwezi wewe kulitenda peke yako. Sikiza sasa neno langu, nitakupa shauri, na Mungu na awe pamoja nawe; uwe wewe kwa ajili ya watu mbele ya Mungu, nawe umletee Mungu maneno yao; nawe utawafundisha zile amri na sheria, nawe utawaonyesha njia ambayo inawapasa kuiendea, na kazi ambayo inawapasa kuifanya. Zaidi ya hayo utajipatia katika watu hawa watu walio na uwezo, wenye kumcha Mungu, watu wa kweli, wenye kuchukia mapato ya udhalimu; ukawaweka juu yao, wawe wakuu wa maelfu, na wakuu wa mia, na wakuu wa hamsini, na wakuu wa kumi; nao wawaamue watu hawa sikuzote; kisha, kila neno lililo kubwa watakuletea wewe, lakini kila neno dogo wataliamua wenyewe; basi kwako wewe mwenyewe utapata nafasi zaidi, nao watauchukua huo mzigo pamoja nawe.”

 

Wasaidizi wa huduma ya kichungaji watafanya majukumu ambayo yangewezwa kufanywa na mchungaji katika kanisa, majukumu hayo ni pamoja na kuwatembelea washirika, kuwasaidia katika maombi, kufanya ufuatiliaji, na kufanya uashauri wa kichungaji, huduma hizi zote zinafanyika chini ya utumishi wa mchungaji kiongozi katika kanisa

 

  1. Kuwahudumia wale wanaotokwa na pepo – watenda kazi, wanafunzi na wenye hekima ni wajibu wao kuhakikisha kuwa mambo yote katika nyumba ya Bwana yanafanyika kwa kufuata utaratibu, Mungu ni Mungu wa utaratibu na anataka mambo yote yafanyike kwa utaratibu, kwa msingi huo, moja ya huduma wanayotakiwa kuifanya ni kuwahudumia wenye kuteswa na mapepo hasa katika ibada za maombezi, wanaousumbuliwa na pepo kama ni wakati ibada inaendelea ni lazima wahamishiwe kwenye vyumba maalumu vya maombezi, lakini kama machungaji yuko katika kuwashughulikia na wanaangushwa au kusumbua miongoni mwa watu watolewe na kupelekwa mbele au sehemu maalumu wanakoweza kuwa na nafasi ya kuhudumiwa na kufunguliwa kanisa linapokuwa tayari na watendakazi wanapokuwa tayari kuhudumu pamoja na Mchungaji na kuhudumu pamoja na Roho wa Mungu kwa utaratibu maalumu, Mungu Roho Mtakatifu atafanya miujiza mikubwa zaidi, kama pepo watasumbua wakati neno la Mungu linaendelea, wenye pepo wapelekwe sehemu nyingine ili neno la Mungu lihubiriwe kwanza, na wasipoteze usikivu!

 

1Wakorintho 14:39-40 “Kwa ajili ya hayo, ndugu, takeni sana kuhutubu, wala msizuie kunena kwa lugha. Lakini mambo yote na yatendeke kwa uzuri na kwa utaratibu.”

 

Waefeso 6:11-12 “Vaeni silaha zote za Mungu, mpate kuweza kuzipinga hila za Shetani. Kwa maana kushindana kwetu sisi si juu ya damu na nyama; bali ni juu ya falme na mamlaka, juu ya wakuu wa giza hili, juu ya majeshi ya pepo wabaya katika ulimwengu wa roho.”

 

Mapepo yanaweza kuwaathiri watu lakini kumbuka kuwa watu sio pepo, kwa hiyo utu wa aliyeathiriwa uthaminiwe na atunzwe kwa heshima zote, tusiwakasirikie wala tusiwe na msisimko ni lazima tuwe wapole na waungwana tuwahifadhi tuwasaidie kufunguka, tuwapeleke sehemu maalumu zilizoainishwa, tuwafute vizuri na tuchukue taarifa zao kwaajili ya ufuatiliaji na kwaajili ya kutunza muujiza na ushuhuda wa baadae

 

Mwondoe mwemye pepo katikati ya umati wa watu, kama ikiwezekana, tumia mamlaka kwa ustaarabu kuyakemea na sio kelele, usitumie nguvu kumbuka pepo wanatoka kwa jina la Yesu na kwa nguvu za Roho Mtakatifu wewe na mimi sio tunaotoa pepo, Pepo wanatolewa na Roho, sisi wajibu wetu ni kuwapa imani na kuwasaidia wao kupokea muujiza wao, msikemee watu wengi pepo mmoja mamlaka moja inatosha.

 

Mathayo 12:28-29 “Lakini mimi nikitoa pepo kwa Roho wa Mungu, basi ufalme wa Mungu umekwisha kuwajilia. Ama awezaje mtu kuingia ndani ya nyumba ya mtu mwenye nguvu na kuviteka vyombo vyake, asipomfunga kwanza yule mwenye nguvu? Ndipo atakapoiteka nyumba yake.”         

 

2Timotheo 2:24 “Tena haimpasi mtumwa wa Bwana kuwa mgomvi; bali kuwa mwanana kwa watu wote, awezaye kufundisha, mvumilivu;”

 

  1. Kuwahudumia watu wanaoangushwa chini – uwe na uwezo wa kutambua ni aina gani ya sababu imempeleka mtu chini, sio kila anayeanguka chini ni kwa sababu ya pepo, wengine wanaweza kuigiza tu, na wengine wanaweza kuwa wamehemewa na hisia kali, na wengine ni kwa sababu ya nguvu za Mungu anaangushwa chini lakini anaweza asiwe na pepo, kwa hiyo usikimbilie kukemea pepo, kwa sababu wengine huangushwa tu na nguvu za Mungu na anaweza kujisikia vibaya kudhaniwa kuwa ana pepo.

 

Luka 5:16-17 “Lakini yeye alikuwa akijiepua, akaenda mahali pasipokuwa na watu, akaomba.Ikawa siku zile mojawapo alikuwa akifundisha, na Mafarisayo na waalimu wa torati walikuwa wameketi hapo, waliotoka katika kila kijiji cha Galilaya, na Uyahudi, na Yerusalemu; na uweza wa Bwana ulikuwapo apate kuponya.”

 

Ufunuo 1:17-18 “Nami nilipomwona, nalianguka miguuni pake kama mtu aliyekufa. Akaweka mkono wake wa kuume juu yangu, akisema, Usiogope, Mimi ni wa kwanza na wa mwisho, na aliye hai; nami nalikuwa nimekufa, na tazama, ni hai hata milele na milele. Nami ninazo funguo za mauti, na za kuzimu.”

 

Wahudumu, watendakazi, wanafunzi na wenye hekima kumbuka ya kuwa lolote linaweza kutokea wakati wa maombezi, na wakati wa ibada jiandae kusimama nyuma kwa huduma, kwa wale wanaohudumiwa,  jiepushe kusukuma watu, tunza heshima ya watu hususani wanawake, wafunike wanapokuwa wamekaa vibaya, hakikisha kunakuwa na utulivu na amani tengeneza mazingira ya Amani, wasaidie kwa upole, omba kimya kimya, na usiwakasirikie wala kuwaudhi wao ni kama wagonjwa wetu na sisi ndio wahudumu wao, jua ya kuwa Mungu ndiye anayewahudumia pamoja nawe kwa sababu hiyo tuwahudumie kwa huruma na upendo

 

  1. Kuwahudumia wageni ambao ni mara yao ya kwanza – Wakristo wanahimizwa kuwa wakarimu, unapowapokea watu vizuri kwa tabasamu la upendo na kuwapa muongozo mzuri, bila papara na kwa kuwaonyesha upendo wao watajua kuwa kweli hapa ni kanisani, kanisani ni mahali ambapo watu wanapaswa kupokelewa kwa upendo kuliko mahali kokote kule, kanisani ni zaidi ya dukani, hotelini, gengeni  na kadhalika waonyeshe watu uungwana mkubwa, msalimie vizuri, mpe ratiba na muelekeo wa ibada,  usimuache akajitenga, zungumza kwa lugha za kawaida, waonyeshe shukurani waonyeshe kuwafuatailia baada ya ibada, wageni wangependa kuagana na mtu yule yule aliyempokea mwanzoni hasa kama ulimpokea vizuri, kwa hiyo yule utakayempokea mwanzoni ni mteja wako mpaka mwisho usimpoteze

 

Waebrania 13:1-2 “Upendano wa ndugu na udumu. Msisahau kuwafadhili wageni; maana kwa njia hii wengine wamewakaribisha malaika pasipo kujua.”

 

Yohana 13:34-35 “Amri mpya nawapa, Mpendane. Kama vile nilivyowapenda ninyi, nanyi mpendane vivyo hivyo. Hivyo watu wote watatambua ya kuwa ninyi mmekuwa wanafunzi wangu, mkiwa na upendo ninyi kwa ninyi.”

 

1Wakorintho 9:19-23 “Maana, ingawa nimekuwa huru kwa watu wote, nalijifanya mtumwa wa wote, ili nipate watu wengi zaidi. Nalikuwa kama Myahudi kwa Wayahudi, ili niwapate Wayahudi; kwa wale walio chini ya sheria, nalikuwa kama chini ya sheria, (ingawa mimi mwenyewe si chini ya sheria), ili niwapate walio chini ya sheria. Kwa wale wasio na sheria nalikuwa kama sina sheria, (si kwamba sina sheria mbele za Mungu, bali mwenye sheria mbele za Kristo), ili niwapate hao wasio na sheria. Kwa wanyonge nalikuwa mnyonge, ili niwapate wanyonge. Nimekuwa hali zote kwa watu wote, ili kwa njia zote nipate kuwaokoa watu. Nami nafanya mambo yote kwa ajili ya Injili ili kuishiriki pamoja na wengine.”          

 

  1. Kuwahudumia viongozi wa serikali – Viongozi wa serikali na viongozi wakubwa wa kitaifa wanaweza kuwa wakristo wenzetu katika kanisa la Mungu lakini pia wanaweza kuwa rafiki zetu na wanaweza kutembelea kanisa letu kwa taarifa au ghafla watendakazi katika kanisa tunapaswa kuwahudumia kwa heshima na ustaarabu pia, heshimu nafasi waliyo nayo lakini usiwaabudu, usilichuje neno la Mungu kwaajili yao, weka heshima sawa na maelekezo ya injili, Mungu hana upendeleo, lakini anayestahili heshima heshima, viongozi wahudumiwe vizuri na kukaribishwa na kama iko sehemu maalumu ya wageni maalumu wanaweza kuelekezwa hapo, kama ni kiongozi mwenye itifaki (Protocol) kadhaa wasikilize viongozi wa itifaki walioambatana naye na shirikiana nao katika utaratibu mzuri, mawasiliano mazuri na kadhalika, kauli za kisiasa kanisani haziruhusiwi, unabii unaohusu wanasiasa, haufai, isipokuwa kama Mungu amesema hivyo, na hakuna sababu za kulazimisha maombi ya kitaifa kama hakukuwa na programu hiyo msibadili gea angani, jiamini, tunza heshima jiepushe na mizaha inayoweza kutafasiriwa vibaya maneno yako yajae neema.

 

Warumi 13:7-8 “Wapeni wote haki zao; mtu wa kodi, kodi; mtu wa ushuru, ushuru; astahiliye hofu, hofu; astahiliye heshima, heshima. Msiwiwe na mtu cho chote, isipokuwa kupendana; kwa maana ampendaye mwenzake ameitimiza sheria.”

 

1Petro 2:17 “Waheshimuni watu wote. Wapendeni ndugu. Mcheni Mungu. Mpeni heshima mfalme

 

Wakolosai 4:5-6. “Enendeni kwa hekima mbele yao walio nje, mkiukomboa wakati. Maneno yenu yawe na neema siku zote, yakikolea munyu, mpate kujua jinsi iwapasavyo kumjibu kila mtu.”  

 

  1. Kuwahudumia watumishi wa Mungu – Watenda kazi, wahudumu, wanafunzi pamoja na wenye hekima katika kanisa wanawajibu pia wa kumuhudumia mchungaji, wakati wote huduma inapoendelea pamoja na shughuli nyingine tutakuwa katika maombi ya kimya kimya tukiendelea kuhudumu pamoja na mtumishi wa Mungu, wafunikwe kwa kuwaombea, uwe na karama ya kupambanua roho na kung’amua kwa haraka watu wanaotaka kuwashambulia watumishi wa Mungu, angalia kama amechoka, angalia kama amekata tamaa, angalia kama anapingwa, angalia kama anahitaji kitambaa cha jasho, maji ya kunywa ama kama analetewa kitu kibaya, wekeni utaratibu wa ulinzi na usalama kwaajili ya kanisa zima na kwaajili ya mtumishi wa Mungu, dhibiti watu kumfikia kwa haraka bila utaratibu, au wale wanaotaka kumshambulia, wekeni timu ya itifaki ya namna ya kumfikia mtumishi wa Mungu, kataza wanaomsengenya, wasahihishe wasiomuelewa, mlinde bila kupigana, muheshimu bila kumuabudu, heshimu mipaka, wajibika kwake, lindeni kile Mungu ameweka ndani yake,  Mke wake na familia yake na kadhalika, tunapowahudumia watumishi wa Mungu tunamuhudumia Mungu pia.

 

Yohana 12:20-21. “Palikuwa na Wayunani kadha wa kadha miongoni mwa watu waliokwea kwenda kuabudu kwenye sikukuu. Basi hao walimwendea Filipo, mtu wa Bethsaida ya Galilaya, wakamwomba, wakisema, Bwana, sisi tunataka kumwona Yesu. Filipo akaenda, akamwambia Andrea; kisha Andrea na Filipo wakamwambia Yesu.”

 

Zaburi 105:14-15”Hakumwacha mtu awaonee, Hata wafalme aliwakemea kwa ajili yao. Akisema, Msiwaguse masihi wangu, Wala msiwadhuru nabii zangu.”

 

1Timotheo 5:17 “Wazee watawalao vema na wahesabiwe kustahili heshima maradufu; hasa wao wajitaabishao kwa kuhutubu na kufundisha

                 

Na. Rev. Innocent Samuel Kamote

Mkuu wa wajenzi mwenye Hekima       

Jumapili, 19 Julai 2026

SHULE YA HUDUMA!


Waefeso 4:11-12 “Naye alitoa wengine kuwa mitume, na wengine kuwa manabii; na wengine kuwa wainjilisti na wengine kuwa wachungaji na waalimu; kwa kusudi la kuwakamilisha watakatifu, hata kazi ya huduma itendeke, hata mwili wa Kristo ujengwe;”



Utangulizi

Shule ya huduma ni mafundisho maalumu ya kibiblia  yaliyoandaliwa  na Rev. Innocent Samuel Kamote kwa kusudi la kuwaadaa watu wa Mungu kuwa tayari kwaajili ya huduma za kichungaji ndani ya kanisa, huduma za kikanisa, na huduma zote za kiroho kupita mafundisho ya Biblia, mafundisho haya huandaliwa kwa programu maalumu zinazolingana na maono ya kanisa letu na mtindo ambao sisi tumechagua kumtumikia Mungu kwa huo, Ni muhimu kujikumbusha kuwa kusudi kubwa la Mungu kutuokoa sio kwaajili ya kuhudhuria ibada makanisani pekee bali kwaajili ya kumtumikia yeye, Mungu anachukizwa sana na wakristo waliodumaa kiroho ambao anawatarajia labda wangelikuwa walimu wa wengine lakini kwa kutokufahamu wao wamebaki kuwa wachanga kwa miaka mingi sasa.

Waebrania 5:11-14 “Ambaye tuna maneno mengi ya kunena katika habari zake; na ni shida kuyaeleza kwa kuwa mmekuwa wavivu wa kusikia. Kwa maana, iwapasapo kuwa waalimu, (maana wakati mwingi umepita), mnahitaji kufundishwa na mtu mafundisho ya kwanza ya maneno ya Mungu; nanyi mmekuwa mnahitaji maziwa wala si chakula kigumu. Kwa maana kila mtu atumiaye maziwa hajui sana neno la haki, kwa kuwa ni mtoto mchanga. Lakini chakula kigumu ni cha watu wazima, ambao akili zao, kwa kutumiwa, zimezoezwa kupambanua mema na mabaya.”

Mungu anapotuokoa anataka tuimarike kwanza kiroho na kisha baada ya kuimarika atutumie sisi kuimarisha wengine, kwa hiyo Mungu hutukuza na kutukomaza kiroho, ili tuje tumtumikie na kuhakikisha kuwa kazi ya huduma inatendeka, kwa hiyo kila mtu aliyeokoka anapaswa kukua na kufikia ngazi ya kuwa mtenda kazi yaani watu wanaowahudumia wengine katika mwili wa Kristo, sio mpango wa Mungu wewe ubaki kama ulivyo kila mwaka!

Luka 22:31-32 “Akasema, Simoni, Simoni, tazama, Shetani amewataka ninyi apate kuwapepeta kama vile ngano; lakini nimekuombea wewe ili imani yako isitindike; nawe utakapoongoka waimarishe ndugu zako.”

Leo tunapochukua muda kuzama kwa kina na mapana na marefu katika kujifunza shule hii maalumu ya huduma, Mungu anataka kukuimarisha na kuleta ufahamu na ukomavu kwako ili wewe uweze kuwa msimamizi wa roho za watu ndani ya kanisa letu na kuwasaidia wengine, tutajifunza somo hili  shule ya huduma kwa kuzingatia vipengele vikuu muhimu vitatu vifuatayo:-


  • Sifa za mwanafunzi wa shule ya huduma.
  • Umuhimu wa kuwa na uzoefu katika huduma.
  • Mambo yatupasayo kufanya kama wahudumu katika kanisa.

 

Sifa za mwanafunzi wa shule ya huduma.

Nyakati za kanisa la kwanza walipochagua watenda kazi walikuwa makini sana kuzingatia sifa  za wale  waliowachagua walijua kuwa wale watakaochaguliwa au kuteuliwa kusaidia kazi mbalimbali wana sifa na vigezo vyenye kuwafaa sana na kuwa wanaaminika na ni wanyenyekevu na watii ambao kupitia wao wataisaidia kazi ya Mungu, na kuwasaidia watu wote walioamini kusimama imara katika Bwana na kuwafundisha wengine kuishika imani vile vile kama wao walivyofundishwa, tunaona kwa mfano Paulo Mtume alimchagua Timotheo mtu ambaye alikuwa anaheshimika sana katika Kanisa  kutokana na usafi wa Imani yake na sifa zake zilijulikana na watu wote wa makanisa yaliyokuwako Listra na Ikonio na baada ya kuongezeka kwake makanisa yakatiwa nguvu katika imani ona:-

Matendo 16:1-5 “Basi akafika Derbe na Listra, na hapo palikuwa na mwanafunzi mmoja jina lake Timotheo, mwana wa mwanamke Myahudi aliyeamini; lakini babaye alikuwa Myunani. Mtu huyo alishuhudiwa vema na ndugu waliokaa Listra na Ikonio.Paulo akamtaka huyo afuatane naye, akamtwaa akamtahiri kwa ajili ya Wayahudi waliokuwako pande zile; kwa maana wote walijua ya kuwa babaye ni Myunani. Basi walipokuwa wakipita kati ya miji ile, wakawapa zile amri zilizoamriwa na mitume na wazee walioko Yerusalemu, ili wazishike. Makanisa yakatiwa nguvu katika ile Imani, hesabu yao ikaongezeka kila siku.”

Ni imani yangu kuwa kila aliyechaguliwa/atakayechaguliwa kuingia katika shule hii ya huduma atakuwa mtii, atakuwa mnyenyekevu, atafuatilia kwa makini mafundisho yetu, na kujitahidi sana kuwa na sifa zinazohitajika sawa na maandiko ili aweze kutumika kwa uaminifu na kupitia wewe makanisa yetu yakatiwe nguvu na kuimarika lakini sio hivyo tu hesabu  ya watu wa makanisa yetu ikaongezeke kila iitwapo leo. Sasa basi mwanafunzi wa shule ya huduma anapaswa kuwa na sifa hizi kama neno la Mungu lisemavyo:-

  1. Kulishika neno la Mungu kama ulivyofundishwa – Mwanafunzi wa shule ya huduma anapaswa kuwa mtu anayeyaamini mafundisho yetu kuyakubali, kuyashahika na kuyafuata vile vile kama alivyofundishwa, mtu hawezi kuwa mwanafunzi wa mtu ambaye hayashiki mafundsho yake, mwanafunzi wetu ni lazima atusome, asome nia ya mitume wa kanisa kuwa wanataka nini wana maono gani na wanaelekea wapi, wanaamini nini, Misingi ya imani yetu ni ipi, kisha aanze kuishi sawa na kile alichojifunza kutoka kwetu na kukisimamia/tetea

 

Yohana 8:31-32 “Basi Yesu akawaambia wale Wayahudi waliomwamini, Ninyi mkikaa katika neno langu, mmekuwa wanafunzi wangu kweli kweli; tena mtaifahamu kweli, nayo hiyo kweli itawaweka huru.”

 

Yohana 14:23-24 “Yesu akajibu, akamwambia, Mtu akinipenda, atalishika neno langu; na Baba yangu atampenda; nasi tutakuja kwake, na kufanya makao kwake. Mtu asiyenipenda, yeye hayashiki maneno yangu; nalo neno mnalolisikia silo langu, ila ni lake Baba aliyenipeleka.”                                

 

Tito 1:7-9 “Maana imempasa askofu awe mtu asiyeshitakiwa neno, kwa kuwa ni wakili wa MUNGU; asiwe mtu wa kujipendeza nafsi yake, asiwe mwepesi wa hasira, asiwe mlevi wala mgomvi, asiwe mpenda mapato ya aibu. Bali awe mkaribishaji, mpenda wema, mwenye kiasi, mwenye haki, mtakatifu, mwenye kudhibiti nafsi yake; akilishika lile neno la imani vile vile kama alivyofundishwa, apate kuweza kuwaonya watu kwa mafundisho yenye uzima, na kuwashinda wenye kupinga.”

 

2Yohana 1:9-10 “Kila apitaye cheo, wala asidumu katika mafundisho ya Kristo, yeye hana Mungu. Yeye adumuye katika mafundisho hayo, huyo ana Baba na Mwana pia. Mtu akija kwenu, naye haleti mafundisho hayo, msimkaribishe nyumbani mwenu, wala msimpe salamu.”

 

Mwanafunzi wetu ni lazima awe yule anayeyashika mafundisho ya Kristo, awe mtu aliyeiva katika neno la Mungu, amejaa neno, analijua neno analipenda anamoyo wa kujifunza na mwenye sifa za kumpenda Yesu huyu anaweza kwenda na kile ambacho Kristo amekikusudia akilishika neno la imani vilevile kama alivyofundishwa!.

 

  1. Awe mwaminifu – Kila mwanafunzi ambaye amechaguliwa au kuteuliwa katika shule ya huduma anapaswa kujifunza kuwa mwaminifu, Imani yangu ni kuwa kila ambaye yuko katika darasa hili atakuwa mwaminifu, na kama hauna uaminifu utaomba Mungu sasa akupe kuwa mwaminifu, Mungu anakuleta katika darasa hili ili akukabidhi injili, na injili inapaswa kukabidhiwa kwa watu waaminifu ambao wana sifa ya kuikabidhi kwa wengine, uaminifu huu unaanzia katika kuhudhuria ibada, zote kufika katika mafundisho ya neno la Mungu, kuandika na kukua kiroho, na kuwa tayari  kuyapeleka hayo katika makanisa yetu yote na nje ya makanisa yetu ili kujenga umoja na afya ya  kiroho inayofanana vile vile sawa na ile aliyotuachia Kristo  na mitume wa Bwana

 

Matendo 2:41-42 “Nao waliolipokea neno lake wakabatizwa; na siku ile wakaongezeka watu wapata elfu tatu. Wakawa wakidumu katika fundisho la mitume, na katika ushirika, na katika kuumega mkate, na katika kusali.”

 

2Timotheo 2:2 “Na mambo yale uliyoyasikia kwangu mbele ya mashahidi wengi, hayo uwakabidhi watu waaminifu watakaofaa kuwafundisha na wengine.”

 

1Wakorintho 4:1-2 “Mtu na atuhesabu hivi, kuwa tu watumishi wa Kristo, na mawakili wa siri za Mungu. Hapo tena inayohitajiwa katika mawakili, ndiyo mtu aonekane kuwa mwaminifu.”

 

Mathayo 24:45-47 “Ni nani basi yule mtumwa mwaminifu mwenye akili, ambaye bwana wake alimweka juu ya nyumba yake, awape watu chakula kwa wakati wake? Heri mtumwa yule, ambaye bwana wake ajapo atamkuta akifanya hivyo.  Amin, nawaambieni, atamweka juu ya vitu vyake vyote.”         

 

  1. Awe na unyenyekevu – Tunapoingia katika shule ya huduma kama hivi, tunaandaliwa kwa lengo, nia na makusudi ya kuwatumikia watu, watu ndio mtaji wetu mkubwa na sio vinginevyo, tunataka roho zao tuzipeleke kwa Kristo kwa ibada na  utumishi wake,  kwa hiyo ni lazima tujifunze unyenyekevu, hatuendi kuwa mabwana wakubwa tunakwenda kuwahudumia watu, Unyeyekevu unapaswa kuwa kama vazi letu iwe ni tabia yetu inayotutambulisha kila mahali, mavazi humtambulisha mtu, watumishi wa Kristo wanapaswa kutambulika kwa unyenyekevu wao kwa sababu ndivyo Bwana wetu Yesu alivyokua na sisi tu mawakili wake

 

Wakolosai 3:12-14 “Basi, kwa kuwa mmekuwa wateule wa Mungu, watakatifu wapendwao, jivikeni moyo wa rehema, utu wema, unyenyekevu, upole, uvumilivu, mkichukuliana, na kusameheana, mtu akiwa na sababu ya kumlaumu mwenzake; kama Bwana alivyowasamehe ninyi, vivyo na ninyi. Zaidi ya hayo yote jivikeni upendo, ndio kifungo cha ukamilifu.”

 

Wafilipi 2:5-8 “Iweni na nia iyo hiyo ndani yenu ambayo ilikuwamo pia ndani ya Kristo Yesu; ambaye yeye mwanzo alikuwa yuna namna ya Mungu, naye hakuona kule kuwa sawa na Mungu kuwa ni kitu cha kushikamana nacho; bali alijifanya kuwa hana utukufu, akatwaa namna ya mtumwa, akawa ana mfano wa wanadamu; tena, alipoonekana ana umbo kama mwanadamu, alijinyenyekeza akawa mtii hata mauti, naam, mauti ya msalaba.”

 

1Petro 5:2-5 “lichungeni kundi la Mungu lililo kwenu, na kulisimamia, si kwa kulazimishwa, bali kwa hiari kama Mungu atakavyo; si kwa kutaka fedha ya aibu, bali kwa moyo. Wala si kama wajifanyao mabwana juu ya mitaa yao, bali kwa kujifanya vielelezo kwa lile kundi. Na Mchungaji mkuu atakapodhihirishwa, mtaipokea taji ya utukufu, ile isiyokauka. Vivyo hivyo ninyi vijana, watiini wazee. Naam, ninyi nyote jifungeni unyenyekevu, mpate kuhudumiana; kwa sababu Mungu huwapinga wenye kiburi, lakini huwapa wanyenyekevu neema.”

 

  1. Awe kielelezo – Katika shule ya huduma kila mwanafunzi anapaswa kudhamiria kuwa kielelezo chema katika Imani yetu na mafundisho yetu, Mungu anapoona kuwa sote tumedhamiria kuwa kielelezo kwa wale watakaoamini ataendelea kutuamini na kutuletea watu wengi zaidi, kwa sababu wanafunzi huigiza kila kitu kinachofanywa na walimu wao, wale tunaowahudumia wataigiza kila kitu kutoka kwetu hivyo neno la Mungu linasiistiza tuwe kielelezo yaani mfano wa kuigwa, wakristo wote watuigize sisi watuone ndio wa kuigizwa na sio wakrito pekee bali kila mahali katika jamii tuwe mfano bora wa kuigwa kwa tabia na mwenendo.

 

Neno kuwa kielelezo katika maandiko ya Kiyunani linatajwa kama neno “tupos” ambalo kwa kiingereza ni “a model for imitation” sawa na mfano wa kuigwa au kielelezo katika Imani, kila muhudumu anapaswa kuwa kielelezo katika usemi, mwenendo imani na usafi hakuna namna ya kukwepa jambo hili.

 

Tito 2:7-8 “katika mambo yote ukijionyesha wewe mwenyewe kuwa kielelezo cha matendo mema, na katika mafundisho yako ukionyesha usahihi na ustahivu, na maneno yenye uzima yasiyoweza kuhukumiwa makosa, ili yule mwenye kupinga atahayarike, kwa kuwa hana neno baya la kunena juu yetu.”

 

1Timotheo 4:12 “Mtu awaye yote asiudharau ujana wako, bali uwe kielelezo kwao waaminio, katika usemi na mwenendo, na katika upendo na imani na usafi.”

 

1Wathesalonike 1:4-7 “Kwa maana, ndugu mnaopendwa na Mungu, twajua uteule wenu; ya kwamba injili yetu haikuwafikia katika maneno tu, bali na katika nguvu, na katika Roho Mtakatifu, na uthibitifu mwingi; kama vile mnavyojua jinsi zilivyokuwa tabia zetu kwenu, kwa ajili yenu. Nanyi mkawa wafuasi wetu na wa Bwana, mkiisha kulipokea neno katika dhiki nyingi, pamoja na furaha ya Roho Mtakatifu. Hata mkawa kielelezo kwa watu wote waaminio katika Makedonia, na katika Akaya.”

 

  1. Nidhamu – Ni muhimu kufahamu kuwa kamwe huwezi kumtenganisha mwanafunzi na maswala ya nidhamu, wanafunzi wa Yesu ni lazima wawe na nidhamu, hii ni sawa na kujitia nidhamu, kuwa na kiasi, kujidhibiti, Neno nidhamu katika kiingereza linatamkwa “Discipline” ambalo kwaa asili linatokana na neno la Kilatini “Discipulus” ambalo maana yake ni “leaner” au “Student”  hii ndio maana ya mzizi wa neno “Disciples” yaani wanafunzi,  kwa msingi huo wanafunzi ni watu wanaojitawala, wanaojitia nidhamu, kama tunataka kumtumikia Mungu kwa kiwango kikubwa na kumpa Mungu nafasi ya kututumia lazima tujitie nidhamu, maisha matakatifu  yanahitaji nidhamu, maombi yanahitaji nidhamu, kujisomea neno kunahitaji nidhamu, kutunza upako kunahitaji nidhamu, kufunga kunahitaji nidhamu, kuabudu kunahitaji nidhamu.

 

1Wakorintho 9:24-27. “Je! Hamjui, ya kuwa wale washindanao kwa kupiga mbio, hupiga mbio wote, lakini apokeaye tuzo ni mmoja? Pigeni mbio namna hiyo, ili mpate. Na kila ashindanaye katika michezo hujizuia katika yote; basi hao hufanya hivyo kusudi wapokee taji iharibikayo; bali sisi tupokee taji isiyoharibika. Hata mimi napiga mbio vivyo hivyo, si kama asitaye; napigana ngumi vivyo hivyo, si kama apigaye hewa; bali nautesa mwili wangu na kuutumikisha; isiwe, nikiisha kuwahubiri wengine, mwenyewe niwe mtu wa kukataliwa.”

               

  1. Upendo kwa watu – Kuna uhusino mkubwa sana kati ya kuhudumia watu na upendo, huduma zote zinazohusisha kuwahudumia watu zinahitaji uwe na upendo, na wala usiwe na ubinafsi, na unapaswa kuwa na huruma kwa watu, upendo huu sio wa hisia  wala wa kinafiki ni utendaji wa kivitendo unaohusisha kukutana na mahitaji ya wengine, kwa hiyo muda wetu, vipawa vyetu tunawekeza katika kuhakikisha tunawahudumia watu kwa huruma na upendo

 

Mathayo 9:35-38 “Naye Yesu alikuwa akizunguka katika miji yote na vijiji, akifundisha katika masinagogi yao, na kuihubiri habari njema ya ufalme, na kuponya magonjwa yote na udhaifu wa kila aina. Na alipowaona makutano, aliwahurumia, kwa sababu walikuwa wamechoka na kutawanyika kama kondoo wasio na mchungaji. Ndipo alipowaambia wanafunzi wake, Mavuno ni mengi, lakini watenda kazi ni wachache. Basi mwombeni Bwana wa mavuno, apeleke watenda kazi katika mavuno yake.”

                               

Umuhimu wa kuwa na uzoefu katika huduma

Ni muhimu kufahamu kuwa nyakati za kanisa la kwanza walipotaka kuchagua mtu katika huduma mojawapo ya msingi waliouzingatia ulikuwa ni uzoefu katika huduma, jambo hili lilikubalika na jamii yote ya wanafunzi, kumtumikia Mungu na kutumikia watu linahesabiwa kama jambo la furaha katika Kristo na sio mzigo kwa sababu iliaminika kama njia ya kujiweka karibu na Mungu huku ukitimiza kazi hii njema ya kiungu

Matendo 1:21-26 “Basi katika watu waliofuatana nasi wakati wote Bwana Yesu alipokuwa akiingia na kutoka kwetu, kuanza tangu ubatizo wa Yohana, hata siku ile alipochukuliwa kwetu kwenda juu, inapasa mmoja wao awe shahidi wa kufufuka kwake pamoja nasi. Wakaweka wawili, Yusufu, aitwaye Barsaba, aliyekuwa na jina la pili Yusto, na Mathiya. Kisha wakaomba, wakasema, Wewe, Bwana, ujuaye mioyo ya watu wote, tuonyeshe ni nani uliyemchagua katika hawa wawili, ashike mahali katika huduma hii na utume huu, alioukosa Yuda, aende zake mahali pake mwenyewe. Wakawapigia kura; kura ikamwangukia Mathiya; naye akahesabiwa kuwa pamoja na mitume kumi na mmoja.”

Tunapozungumzia uzoefu hapa tunamaanisha mtu aliyekaa katika mafundisho ya Bwana Yesu kwa muda wa kutosha au aliyepitia shule zote muhimu zinazohusiana na utumishi huu tulioitiwa, kwa maana nyingine hapaswi kuwa mtu aliyeokoka hivi karibuni au aliyepandishwa kwa haraka haraka, kanisa la sasa lina watu wengi walioibuka kama uyoga, mtu alikuwa mganga wa kienyeji, mchawi, sheikh hata hajakaa sawa tayari kesho unasikia ni mhudumu

1Timotheo 3:6-7 “Wala asiwe mtu aliyeongoka karibu, asije akajivuna akaanguka katika hukumu ya Ibilisi. Tena imempasa kushuhudiwa mema na watu walio nje; ili asianguke katika lawama na mtego wa Ibilisi.”

Kanisa linalotaka uamsho mzito  na wa kudumu halina budi kwenda na msingi huu, ambapo neno la Mungu linaonya kuwa hatupaswi kumchagua mtu katika huduma ambaye bado ni mchanga, kumpaisha mtu kwa haraka kunaweza kutuletea madhara makubwa kutokana na kuwa mtu huyo anaweza asiwe na uzoefu wa ukomavu wa kiroho, kwa hiyo kumuinua mtu kwa haraka kunaweza kumletea kiburi na majivuno na anguko la haraka pia kama Shetani alivyoanguka kwa majivuno, kwa hiyo mwanafunzi anayeandaliwa kuwa mhudumu wa injili anapawa kuwa mtu mzima kiroho mtu aliyepitishwa na Mungu katika shule mbalimbali na sio kwa sababu ya kipawa chake  kuepusha hatari ya kuwa na majivuno kwa hiyo asiwe mtu mchanga au aliyeinuka haraka “Novice”  kwa Kiyunani “neophutos” maana yake kwa kingereza ni “Newly planted” yaani pandikizi jipya mtu ambaye hana ukomavu katika imani, kwa hiyo anaweza kuwa ameokoka hivi karibuni, au akawa mtu ambaye amedumaa kiroho, ndio maana siku hizi unaweza kuona mtu ni Askofu lakini ana bifu na mtu fulani, anabagua ana mtu ana uadui naye, ana uchungu, na ugomvi na kupoozesha kabisa sifa zinazomuonyesha kuwa ni mwanafunzi wa Yesu, makanisa mengi yamepoteza mwelekeo pale yalipowababaikia watu kwa sababu walikuwa Masheihk, au Wasomi, au wenye vyeo vikubwa na bila kupitia michakato kadhaa ya kiimani wakapaishwa kuwa viongozi wa kanisa na hii imechangia kuilifanya kanisa kupoa na kuwa na watu wenye kutumia akili zao zaidi kuliko hata kumsikiliza Mungu Roho Mtakatifu japo tunahitaji uwiano.

Onyo la kutokuweka viongozi wachanga katika kanisa linatolewa katika misingi mikuu minne ya tahadhari:-

  1. Kuanguka katika mtego wa ibilisi kuwa na kiburi
  2. Kuitia aibu kanisa kutokana na kukosa ukomavu na mizizi ya kiimani
  3. Kukosekana kwa msimamo katika mafundisho na kushindwa kuisimamia imani au kuitetea
  4. Kwamba bado anahitaji ukomavu katika wokovu,mafundisho na tabia, ukomavu wa hekima na busara

 

Matendo 6:3-4 “Basi ndugu, chagueni watu saba miongoni mwenu, walioshuhudiwa kuwa wema, wenye kujawa na Roho, na hekima, ili tuwaweke juu ya jambo hili; na sisi tutadumu katika kuomba na kulihudumia lile Neno.”

Ukomavu wa kiroho ni mchakato unachukua muda, wokovu ni mara moja lakini kujengeka kiroho ni safari inayohitaji mchakato wa muda mpaka mtu akue afikie hatua ya kuweza kula chakula kigumu, wakati mtoto mchanga kiroho anahitaji maziwa na huduma ya kichungaji, mtoto mdogo anahitaji malezi na sio kubebeshwa mzigo, kuwabebesha watoto wachanga kiroho mzigo wa uongozi ni kutafuta kuwadhuru na kuwaharibu na pia kuliharibu kanisa, unaweza kuwafanya wawe na kiburi na majivuno, unaweza kusababisha imani yao ikaharibika, unaweza kuwafanya wakakata tamaa,angalau mtu awe amedumu katika Imani na mafundisho kwa muda usiopungua miaka mitatu kama alikuwa mwaminifu kuhuduhria ibada na mafundisho ya kanisa letu, anaijua imani yetu na anauwezo wa kuitetea.

Waebrania 5:14 “Lakini chakula kigumu ni cha watu wazima, ambao akili zao, kwa kutumiwa, zimezoezwa kupambanua mema na mabaya.”

1Wakorintho 3:1-2 “Lakini, ndugu zangu, mimi sikuweza kusema nanyi kama na watu wenye tabia ya rohoni, bali kama na watu wenye tabia ya mwilini, kama na watoto wachanga katika Kristo. Naliwanywesha maziwa sikuwalisha chakula; kwa kuwa mlikuwa hamjakiweza. Naam, hata sasa hamkiwezi,”

1Timotheo 3:8-10 “Vivyo hivyo mashemasi na wawe wastahivu; si wenye kauli mbili, si watu wa kutumia mvinyo sana, si watu wanaotamani fedha ya aibu. Wakiishika siri ya imani katika dhamiri safi.Hawa pia na wajaribiwe kwanza; baadaye waitende kazi ya shemasi, wakiisha kuonekana kuwa hawana hatia.”

Mambo yatupasayo kufanya kama wahudumu katika kanisa.

Kila mwanafunzi wa shule ya huduma anapaswa kufahamu kuwa ameitwa kuutumikia mwili wa Kristo huu ni utu mishi mwema sana na wa hali ya juu na kama kila mmoja atakuwa mwaminifu Mungu atampa thawabu, kwa hiyo huduma hii iko kwaajili ya kufaidiana yaani kuujenga mwili wa Kristo na sio kushindana na uongozi, bali kusaidia.

1Wakorintho 12:4-7 “Basi pana tofauti za karama; bali Roho ni yeye yule. Tena pana tofauti za huduma, na Bwana ni yeye yule. Kisha pana tofauti za kutenda kazi, bali Mungu ni yeye yule azitendaye kazi zote katika wote. Lakini kila mmoja hupewa ufunuo wa Roho kwa kufaidiana.”

Neno kufaidiana katika maandiko ya kiyunani linatumika neno “Sumpherōambalo kwa kiingereza linatumika neno “Contribute” sawa na kuchangia kwa faida kama vile Paulo alivyosema mahali Fulani mmoja alipanda mwingine akatia maji bali mwenye kukuza ni Mungu, Mungu ametupa huduma na akili na vipawa mbalimbali ili viweze kuchangia katika kuujenga mwili wa Kristo ambao kimsingi hauwezi kujengwa na mtu mmoja kwa sababu hiyo tuhudumiane kwa Upendo.

Wagalatia 5:13 “Maana ninyi, ndugu, mliitwa mpate uhuru; lakini uhuru wenu usiwe sababu ya kuufuata mwili, bali tumikianeni kwa upendo.”

Kila mwanafunzi wa shule ya huduma anapaswa kufahamu kuwa ameitwa kwaajili ya kuwatia nguvu wengine, kufarijiana, kujengana na kunoana, kumbuka kuwa chuma hunoa chuma!

1Wathesalonike 5:9-11. “Kwa kuwa Mungu hakutuweka kwa hasira yake, bali tupate wokovu, kwa Bwana wetu Yesu Kristo; ambaye alikufa kwa ajili yetu, ili tuishi pamoja naye, kwamba twakesha au kwamba twalala. Basi, farijianeni na kujengana kila mtu na mwenzake, vile vile kama mnavyofanya.”

Kila mwanafunzi wa shule ya huduma anapaswa kufahamu kuwa anapaswa kusaidia huduma ya kichungaji, karama za huduma tulizo nazo ni huduma za masaidiano kwa hiyo katika kanisa tunawasaidia viongozi wetu katika kubeba maono, kulinda umoja na kusaidia kazi za kichungaji        

Warumi 12:4-8 “Kwa kuwa kama vile katika mwili mmoja tuna viungo vingi, wala viungo vyote havitendi kazi moja; Vivyo hivyo na sisi tulio wengi tu mwili mmoja katika Kristo, na viungo, kila mmoja kwa mwenzake. Basi kwa kuwa tuna karama zilizo mbalimbali, kwa kadiri ya neema mliyopewa; ikiwa unabii, tutoe unabii kwa kadiri ya imani; ikiwa huduma, tuwemo katika huduma yetu; mwenye kufundisha, katika kufundisha kwake; mwenye kuonya, katika kuonya kwake; mwenye kukirimu, kwa moyo mweupe; mwenye kusimamia kwa bidii mwenye kurehemu, kwa furaha.”

 

Na. Rev. Innocent Samuel Kamote.

 

Mkuu wa wajenzi mwenye Hekima