Luka 8:1-3. “Ikawa baada ya hayo alikuwa
akizunguka-zunguka katika miji na vijiji akihubiri na kuitangaza habari njema
ya ufalme wa Mungu; na wale Thenashara walikuwa pamoja naye, na wanawake kadha
wa kadha ambao walikuwa na pepo wabaya na magonjwa wakaponywa; nao ni Mariamu
aitwaye Magdalene aliyetokwa na pepo saba, na Yoana mkewe Kuza, wakili wake
Herode, na Susana, na wengine wengi, waliokuwa wakimhudumia kwa mali zao.”
Utangulizi:
Ni muhimu kufahamu kwamba Kanisa
lisipowatambua wanawake kama sehemu muhimu ya huduma linaweza kupoteza sehemu
kubwa sana ya nguvu zake ambazo Mungu ameziweka katika mwili wa Kristo,
Maandiko yanaonyesha kuwa nyakati za Biblia wanawake hawakuwa watazamaji tu wa
maswala ya imani na badala yake walikuwa mstari wa mbele katika kumtumikia
Mungu kwa maombi, kushuhudia, kulea, kufundisha na kuihubiri injili, lakini sio
hivyo tu walimtumikia Mungu kwa huduma na kwa kutoa mali zao na kuwa sehemu
muhimu na baraka kubwa sana kwa injili.
Marko 15:40-41 “Palikuwako na wanawake
wakitazama kwa mbali; miongoni mwao alikuwamo Mariamu Magdalene, na Mariamu
mama yao Yakobo mdogo na Yose, na Salome;hao ndio waliofuatana naye huko
Galilaya, na kumtumikia; na wengine wengi waliopanda pamoja naye mpaka
Yerusalemu.”
Unaona tunajifunza hapo kwamba
wanawake waliookoka sio watu wanaopaswa kukaa tu kanisani bila kufanya kitu,
wanawake nao wanapaswa kumtumikia Mungu na kushiriki bega kwa bega katika
huduma huku wakitumia karama zao, wito, mzigo waliopewa kutimiza jukumu walilopewa
katika ufalme wa Mungu, wanawake waliomwamini Yesu walianza kumtumikia mara
moja hata kabla ya kuanza kwa kanisa, walishirikiana naye kwa hali na mali, na
bega kwa bega kusaidia huduma, Kwa msingi huo basi leo katika maswala ya huduma
tutajifunza somo hili muhimu Huduma ya
wanawake Katika Kanisa! Kwa kuzingatia vipengele vikuu muhimu vitatu
viafuatavyo:-
·
Umuhimu
wa huduma ya wanawake katika Kanisa.
·
Huduma ya
wanawake katika kanisa.
·
Mambo
yanayoweza kufanywa na wanawake katika jamii ya kanisa.
Umuhimu wa huduma ya
wanawake katika Kanisa
Huduma ya wanawake katika kanisa
kwa ujumla tunazungumzia ushiriki wa mwanamke katika kulitimiza au kutekeleza
agizo kuu la Bwana wetu Yesu Kristo, na katika kuujenga mwili wa Kristo,
wanawake ni nyenzio Muhimu katika huduma na katika kuendeleza kazi ya Mungu
duniani sawasawa na karama walizopewa, wakati Yoeli anatabiri kuhusu kuachiliwa
kwa Roho Mtakatifu kwaajili ya utumishi kila kundi liliguswa kama watumishi wa
Mungu wakiwepo wanawake:-
Yoel 2:28-30 “Hata itakuwa, baada ya hayo,
ya kwamba nitamimina roho yangu juu ya wote wenye mwili; na wana wenu, waume
kwa wake, watatabiri, wazee wenu wataota ndoto, na vijana wenu wataona maono;
tena juu ya watumishi wenu, wanaume kwa wanawake, katika siku zile, nitamimina roho
yangu. Nami nitaonyesha mambo ya ajabu katika mbingu na katika dunia, damu, na
moto, na minara ya moshi.”
Kwa sababu hiyo Wanawake ni
sehemu muhimu ya dunia hii, ni sehemu muhimu ya uumbaji wa Mungu na waliumbwa
kwa kusudi kubwa la kipekee katika mpango wa Mungu na ni wasaidizi wa ajabu sana
kwa sababu hiyo wanahusika katika kusudi na mpango wa Mungu si kama watu wa
pembeni bali kama watu wanaojumuishwa kwa umuhimu wao katika jamii kumletea
Mungu utukufu, uko ukweli usio wa kitafiti ya kwamba mtumishi wa Mungu awaye
yote anapoanza Kanisa utaweza kuona wenye kuonyesha muitikio kwa injili kwa
haraka zaidi ni wanawake na wao hufanya idadi kubwa ya washirika kanisani na
kwa sababu hiyo karibu nusu na zaidi ya idadi ya washirika katika kanisa ni
wanawake sasa basi tunawezaje kuwapuuzia watumishi hawa wa Mungu ambao
hawabaguliwi kwa lolote katika maandiko?
Wagalatia 3:26-29 “Kwa kuwa ninyi nyote
mmekuwa wana wa Mungu kwa njia ya imani katika Kristo Yesu. Maana ninyi nyote
mliobatizwa katika Kristo mmemvaa Kristo. Hapana Myahudi wala Myunani. Hapana
mtumwa wala huru. Hapana mtu mume wala mtu mke. Maana ninyi nyote mmekuwa mmoja
katika Kristo Yesu. Na kama ninyi ni wa Kristo, basi, mmekuwa uzao wa Ibrahimu,
na warithi sawasawa na ahadi.”
Kwa msingi huu pamoja na changamoto
za kiutamaduni kuhusu wanawake, ukweli unabaki wazi kuwa wao ni sehemu kubwa ya
kanisa, wahudhuriaji wazuri wa ibada, wako mstari wa mbele katika kuipokea
imani na hivyo inaweza kuwa hasara kubwa sana kama hatutawekeza injili na
mafundisho kwao kwa sababu Mungu hajawahi kuwapuuzia katika mpango wake wa
ukombozi kwa mwanadamu hata ahadi ya ukombozi wa Mwanadamu walipewa
Tito 2:1-5 “Lakini wewe nena mambo yapasayo
mafundisho yenye uzima; ya kwamba wazee wawe wenye kiasi, wastahivu, wenye
busara, wazima katika imani na katika upendo na katika saburi. Vivyo hivyo na
wazee wa kike wawe na mwenendo wa utakatifu; wasiwe wasingiziaji, wasiwe wenye
kutumia mvinyo nyingi, bali wafundishao mema; ili wawatie wanawake vijana
akili, wawapende waume zao, na kuwapenda watoto wao; na kuwa wenye kiasi, kuwa
safi, kufanya kazi nyumbani mwao, kuwa wema, kuwatii waume zao wenyewe; ili
neno la Mungu lisitukanwe.”
Huduma ya wanawake katika jamii
na kanisa inaweza kuwa na mkono mrefu zaidi katika kurahisisha huduma ya
kichungaji hata kwa kuyafikia mahitaji muhumu ya kimwili na kisaokolojia ya
wanawake, utafiti unathibitisha ya kuwa asilimia 73% ya mahitaji ya kiroho na kijamii ya wanawake yanaweza
kuratibiwa na kuhudumiwa na wanawake kwa kiwango kikubwa zaidi, mfano
changamoto za Mimba kuharibika, kuhudumia mwanamke aliyebakwa, kuhudumia wenye ukomo
wa siku za hedhi, hoja za ukatili wa majumbani, maswala ya ndoa, maswala ya
kuvurugika kwa homoni, huduma za kujifungua, mfadhaiko wa wanawake, changamoto
za kutokwa na damu, wakati mwingine hayawezi kutatuliwa wala kushughulikiwa
vizuri na kwa ubora na watumishi wa kiume, na wanawake wenyewe pia wanaweza
kujisikia aibu kujielezea vizuri kwa watumishi wanaume na hivyo mwanamke
anahitajika asimame katika nafasi yake ili kusaidia kuyafikia mambo ya kike
katika jamii, kwa msingi huo utakubaliana nami pia kuwa wanawake wanahitajika
na wana wajibu mkubwa wa kuitikia wito wa kupata ufahamu na kutumika na kamwe
tusiwabague.
Huduma ya wanawake
katika kanisa
Luka 8:1-3. “Ikawa baada ya hayo alikuwa
akizunguka-zunguka katika miji na vijiji akihubiri na kuitangaza habari njema
ya ufalme wa Mungu; na wale Thenashara walikuwa pamoja naye, na wanawake kadha
wa kadha ambao walikuwa na pepo wabaya na magonjwa wakaponywa; nao ni Mariamu
aitwaye Magdalene aliyetokwa na pepo saba, na Yoana mkewe Kuza, wakili wake
Herode, na Susana, na wengine wengi, waliokuwa wakimhudumia kwa mali zao.”
Katika nyakati za zamani hususani
nyakati za karne ya kwanza wanawake hawakupewa kipaumbele sana katika jamii
nyingi duniani ikiwepo jamii ya Kiyahudi, wanawake walikuwa na nafasi ndogo
sana katika shughuli za kijamii na kielimu na hata kihuduma, hata hivyo tunaona
Mungu aliwapa nafasi ya kutumika na Pia Bwana Yesu, akiwafundisha kuwahudumia,
kuwaponya na hata kuwaacha wafuatane naye katika huduma huku wakifanya utumishi
wao kumuhudumia Bwana Yesu. Katika andiko la Msingi wanatajwa Mariam Magdalene,
Yoana, Susana na wanawake wengine wengi waliomtumikia Yesu na wanafunzi wake
tena walitumia mali zao, sio hivyo tu wanawake wengi walitumiwa kwa kazi
mbalimbali wakitumiwa kama Baraka katika jamii na wahusika wakuu katika imani,
wako wanawake wengi lakini hapa tutaangalia wachache tu kama sehemu ya mfano:-
Debora – Moja ya waamuzi muhimu sana ambaye alikuwa wa kiroho zaidi
ya waamuzi wote wanaotajwa katika maandiko, mwanamke huyu aliwamua Israel lakini
pia alikuwa ni nabii aliyetambua mapenzi ya Mungu na kujua nini kinachopaswa
kufanyika, alimtia moyo Baraka kupigana vita ya ukombozi dhidi ya uonevu wa
watu wa Mungu ona
Waamuzi 4:4-9 “Basi Debora, nabii mke,
mkewe Lapidothi, ndiye aliyekuwa mwamuzi wa Israeli wakati ule. Naye alikaa
chini ya mtende wa Debora, kati ya Rama na Betheli, katika nchi ya vilima
vilima ya Efraimu; wana wa Israeli wakakwea kwake, awaamue. Huyo akatuma mtu
akamwita Baraka wa Abinoamu toka Kedesh-Naftali, akamwambia, Je! Bwana, Mungu
wa Israeli, hakutoa amri, akisema, Enenda, ukawavute kwako, huko katika mlima
wa Tabori, watu elfu kumi wa wana wa Naftali, na wa wana wa Zabuloni? Nami
nitakuvutia Sisera, amiri wa jeshi lake Yabini, hata mto wa Kishoni, pamoja na
magari yake, na wingi wa watu wake; nami nitamtia mkononi mwako. Baraka akamwambia,
Kama utakwenda pamoja nami ndipo nitakwenda; bali kama huendi pamoja nami, mimi
siendi. Basi akasema, Hakika nitakwenda pamoja nawe, lakini safari
utakayoiendea haitakupatia heshima wewe; maana Bwana atamwuza Sisera katika
mkono wa mwanamke. Debora akainuka, akaenda pamoja na Baraka mpaka Kedeshi.”
Esta – Anakumbukwa kama mwanamke shujaa aliyesimama mstari wa mbele
katika kuwakomboa na kuhakikisha usalama wa wayahudi huko Shushani Ngomeni,
alihatarisha maisha yake, alifunga na kuomba alijitia ujasiri lakini alikuwa
tayari kuangamia kwaajili ya jamii ya watu wake Mungu alimtumia kama mkombozi
aliyewasaidia Wayahudi
Esta 4:13-16 “Naye Mordekai akawaagiza
wampelekee Esta jibu la kusema, Wewe usijidhanie kuwa wewe utaokoka nyumbani
mwa mfalme, zaidi ya Wayahudi wote. Kwa maana wewe ukinyamaza kabisa wakati
huu, ndipo kutakapowatokea Wayahudi msaada na wokovu kwa njia nyingine; ila
wewe utaangamia pamoja na mlango wote wa baba yako; walakini ni nani ajuaye
kama wewe hukuujia ufalme kwa ajili ya wakati kama huo? Basi Esta akawatuma ili
wamjibu Mordekai, Uende ukawakusanye Wayahudi wote waliopo hapa Shushani,
mkafunge kwa ajili yangu; msile wala kunywa muda wa siku tatu, usiku wala mchana,
nami na wajakazi wangu tutafunga vile vile; kisha nitaingia kwa mfalme, kinyume
cha sheria; nami nikiangamia, na niangamie.”
Mariam mama yake Yesu – Ni mwanamke mwenye moyo wa kishujaa,
aliyekubali kubeba mimba katika mazingira ya tamaduni ngumu sana na hivyo
kuhatarisha maisha yake ndoa yake na kustahimili aibu ya uanawali wake kwa
sababu ya kukubali kujitoa kubeba kusudi la Mungu kwa kukubali kumbeba mwokozi
wa ulimwengu huu tumboni mwake (kumbuka
ilikuwa ngumu sana kueleweka kuwa ana mimba kwa uwezo wa Roho Mtakatifu)
Luka 1:26-38 “Mwezi wa sita, malaika
Gabrieli alitumwa na Mungu kwenda mpaka mji wa Galilaya, jina lake Nazareti,
kwa mwanamwali bikira aliyekuwa ameposwa na mtu, jina lake Yusufu, wa mbari ya
Daudi; na jina lake bikira huyo ni Mariamu. Akaingia nyumbani kwake akasema,
Salamu, uliyepewa neema, Bwana yu pamoja nawe. Naye akafadhaika sana kwa ajili
ya maneno yake, akawaza moyoni, Salamu hii ni ya namna gani? Malaika
akamwambia, Usiogope, Mariamu, kwa maana umepata neema kwa Mungu. Tazama,
utachukua mimba na kuzaa mtoto mwanamume; na jina lake utamwita Yesu. Huyo
atakuwa mkuu, ataitwa Mwana wa Aliye juu, na Bwana Mungu atampa kiti cha enzi
cha Daudi, baba yake. Ataimiliki nyumba ya Yakobo hata milele, na ufalme wake
utakuwa hauna mwisho. Mariamu akamwambia malaika, Litakuwaje neno hili, maana
sijui mume? Malaika akajibu akamwambia, Roho Mtakatifu atakujilia juu yako, na
nguvu zake Aliye juu zitakufunika kama kivuli; kwa sababu hiyo hicho
kitakachozaliwa kitaitwa kitakatifu, Mwana wa Mungu. Tena, tazama, jamaa yako
Elisabeti naye amechukua mimba ya mtoto mwanamume katika uzee wake; na mwezi
huu ni wa sita kwake yeye aliyeitwa tasa; kwa kuwa hakuna neno lisilowezekana
kwa Mungu. Mariamu akasema, Tazama, mimi ni mjakazi wa Bwana; na iwe kwangu kama
ulivyosema. Kisha malaika akaondoka akaenda zake.”
Lidia – Mwanamke wa kwanza kupokea injili kule Ulaya, yeye
aliishikia injili na kuyatunza maneno ya Bwana, alikuwa mtu muelewa na
aliwakaribisha wahubiri wa injili nyumbani kwake na kuruhusu kazi ya huduma
ifanyike kule Makedonia
Matendo 16:13-15 “Hata siku ya sabato
tukatoka nje ya lango, tukaenda kando ya mto, ambapo tukadhani ya kuwa pana
mahali pa kusali; tukaketi, tukasema na wanawake waliokutana pale. Mwanamke
mmoja, jina lake Lidia, mwenye kuuza rangi ya zambarau, mwenyeji wa Thiatira,
mcha Mungu, akatusikiliza, ambaye moyo wake ulifunguliwa na Bwana, ayatunze
maneno yaliyonenwa na Paulo. Hata alipokwisha kubatizwa, yeye na nyumba yake,
akatusihi, akisema, Kama mmeniona kuwa mwaminifu kwa Bwana, ingieni nyumbani
mwangu mkakae. Akatushurutisha.”
Prisila – Alikuwa ni mwanamke mtenda kazi pamoja na Paulo Mtume
yeye na mumewe Akila na anaonekana kuwa alikuwa mwalimu mzuri sana wa neno la
Mungu wao walimsaidia Apolo moja ya walimu maarufu sana wa nyakati za kanisa la
Kwanza kuijua njia ya Mungu kwa usahihi zaidi hivyo kuiboresha huduma yake kwa
kiwango kikubwa sana na katika jamii ya makanisa
Matendo 18:24-28 “Basi Myahudi mmoja, jina
lake Apolo, mzalia wa Iskanderia, mtu wa elimu, akafika Efeso; naye alikuwa
hodari katika maandiko. Mtu huyo alikuwa amefundishwa njia ya Bwana; na kwa
kuwa roho yake ilikuwa ikimwaka, alianza kunena na kufundisha kwa usahihi
habari za Yesu; naye alijua ubatizo wa Yohana tu. Akaanza kunena kwa ujasiri
katika sinagogi; hata Prisila na Akila walipomsikia wakamchukua kwao,
wakamweleza njia ya Bwana kwa usahihi zaidi. Na alipotaka kuvuka bahari aende
mpaka Akaya, ndugu wakamhimiza, wakawaandikia wale wanafunzi wamkaribishe, naye
alipofika akawasaidia sana wale waliokwisha kuamini kwa neema ya Mungu. Kwa
maana aliwashinda Wayahudi kabisa kabisa mbele ya watu wote, akionyesha kwa
maneno ya maandiko ya kuwa Yesu ni Kristo.”
Kwa ujumla tungeweza kuona
wanawake wengi sana na mchango wao mkubwa katika imani na jinsi Mungu alivyowatumia
kwa shughuli mbalimbali za kiimani, kubwa zaidi tunajifunza ya kuwa Mungu
anawatumia wanawake katika kila kizazi bila kuwapuuzia kusimamia wajibu wa
kibiblia na kihuduma katika kuifanikisha kazi hii iliyo njema ya Mungu na
ufalme wake, kwa sababu hiyo kanisa halipaswi kupuuzia umahiri wa wanawake
katika utumishi wa aina mbalimbali na kwa sababu hiyo tuwahimize, tuwafundishe
na tuwaamini na kutambua mchango wao
katika maeneo mbali mbali ya kihuduma hata yale yasiyoonekana
Mambo yanayoweza
kufanywa na wanawaje katika jamii ya kanisa
Luka 8:1-3. “Ikawa baada ya hayo alikuwa
akizunguka-zunguka katika miji na vijiji akihubiri na kuitangaza habari njema
ya ufalme wa Mungu; na wale Thenashara walikuwa pamoja naye, na wanawake kadha
wa kadha ambao walikuwa na pepo wabaya na magonjwa wakaponywa; nao ni Mariamu
aitwaye Magdalene aliyetokwa na pepo saba, na Yoana mkewe Kuza, wakili wake
Herode, na Susana, na wengine wengi, waliokuwa wakimhudumia kwa mali zao.”
Wanawake ni watoaji – Moja ya utumishi mkubwa walionao wanawake na
ambao wanaweza kuufanya kwa kiwango kikubwa sana kwa asili na kivitendo ni
Kumuhudumia Mungu kwa mali zao, unaweza kuona katika huduma ya Bwana Yesu
wanawake kadhaa wanatajwa hapo na wengine wengi na Luka anahitimisha kwa
kuonyesha kuwa walikuwa wakimuhudunia Mungu kwa mali zao, hii ni ishara ya dhahiri
kuwa unapozungumzia swala la utoaji unaweza kuona wanawake wanaongoza kwa
utoaji makanisani na katika maandiko hata kuliko wanaume kimaumbile na kwa
kadiri ya mkao wa moyo wao, Biblia imejaa mifano kadhaa ya wanawake
waliojihusisha na utoaji katika Biblia wakiwemo:-
· Mwanamke
mmoja mjane – Mwanamke mmoja aliyetoa senti ndogo sana na ya mwisho katika
sadaka yake wakati Yesu anafuatilia utoaji hekaluni, aliuona Moyo wa mwanamke
huyu kuwa ingawa alikuwa masikini na hakuwa na kitu lakini alijitoa kwa moyo
wake wote kile kidogo alichokuwa nacho kwa sababu ya upendo wake mkubwa kwa
Mungu ona:-
Marko 12:41-44
“Naye akaketi kulielekea sanduku la hazina,
akatazama jinsi mkutano watiavyo mapesa katika sanduku. Matajiri wengi wakatia
mengi. Akaja mwanamke mmoja, mjane, maskini, akatia senti mbili, kiasi cha nusu
pesa. Akawaita wanafunzi wake, akawaambia, Amin, nawaambia, Huyu mjane maskini
ametia zaidi kuliko wote wanaotia katika sanduku la hazina; maana hao wote
walitia baadhi ya mali iliyowazidi; bali huyu katika umaskini wake ametia vyote
alivyokuwa navyo, ndiyo riziki yake yote pia.”
· Mwanamke
mjane wa Sarepta – Ni mwanamke ambaye hakuwa na kitu kikubwa sana lakini
alikuwa na moyo wa utoaji, Moyo wa kumtolea Bwana na kuweka kipaumbele maswala
ya Mtumishi wake, hakuwa na ubinafsi alimheshimu mtumishi wa Mungu Eliya, na
mwanamke huyu Mungu mwenyewe alisema amemwagiza amlishe mtumishi wake utoaji
wake wa kimuujiza ulimfanya mwanamke huyu asipungukiwe na kitu kwa muda mrefu
1Wafalme
17:8-16 “Neno la Bwana likamjia, kusema, Ondoka,
uende Sarepta, ulio mji wa Sidoni, ukae huko. Tazama, nimemwagiza mwanamke
mjane wa huko akulishe. Basi, akaondoka, akaenda Sarepta; hata alipofika
langoni pa mji, kumbe! Mwanamke mjane alikuwako akiokota kuni; akamwita,
akamwambia, Niletee, nakuomba, maji kidogo chomboni nipate kunywa. Alipokuwa
akienda kuleta, akamwita akasema, Niletee, nakuomba, kipande cha mkate mkononi
mwako. Naye akasema, Kama Bwana, Mungu wako, aishivyo, sina mkate, ila konzi ya
unga katika pipa, na mafuta kidogo katika chupa; nami ninaokota kuni mbili ili
niingie nijipikie nafsi yangu na mwanangu, tuule tukafe. Eliya akamwambia,
Usiogope; enenda ukafanye kama ulivyosema; lakini unifanyie kwanza mkate mdogo
ukaniletee; kisha ujifanyie nafsi yako na mwanao. Kwa kuwa Bwana, Mungu wa
Israeli, asema hivi, Lile pipa la unga halitapunguka, wala ile chupa ya mafuta
haitaisha, hata siku ile Bwana atakapoleta mvua juu ya nchi. Basi akaenda,
akafanya kama alivyosema Eliya; na yeye mwenyewe, na Eliya, na nyumba yake,
wakala siku nyingi. Lile pipa la unga halikupunguka, wala ile chupa ya mafuta
haikuisha, sawasawa na neno la Bwana alilolinena kwa kinywa cha Eliya.”
· Mwanamke
Mshunami – alikuwa ni mwanamke mwenye ukarimu, aliamua kumkarimu mtumishi
wa Mungu Elisha na kumuhudumia kwa chakula na hata kumjengea chumba maalumu cha
mapumziko awapo safarini mwanamke huyu alikuwa na imani kuwa mtu yule ni mtu wa
Mungu na anastahili kukirimiwa kama Huduma.
2Wafalme 4:8-17
“Hata ikawa siku moja, Elisha alikwenda Shunemu; na
huko kulikuwa na mwanamke mmoja mwenye cheo; naye akamshurutisha aje ale
chakula. Ikawa kila alipopita njia ile, huingia kula chakula. Yule mwanamke
akamwambia mumewe, Tazama, mimi naona ya kuwa mtu huyu apitaye kwetu mara kwa
mara ni mtu mtakatifu wa Mungu. Nakuomba, tumfanyie chumba kidogo ukutani; na
ndani yake tumwekee kitanda, na meza, na kiti, na kinara cha taa; na itakuwa,
atujiapo, ataingia humo. Ikawa siku moja akafika huko, akaingia katika chumba
kile akalala. Akamwambia Gehazi mtumishi wake, Mwite yule Mshunami. Naye alipokwisha
kuitwa, akasimama mbele yake. Akamwambia, Sema naye sasa, Tazama, wewe
umetutunza sana namna hii; utendewe nini basi? Je! Uombewe neno kwa mfalme, au
kwa amiri wa jeshi? Yule mwanamke akamjibu, Mimi ninakaa katika watu wangu
mwenyewe. Akasema, Basi, atendewe nini? Gehazi akajibu, Hakika hana mwana, na
mumewe ni mzee. Akamwambia, Kamwite. Naye alipokwisha kuitwa, akasimama
mlangoni. Akasema, Panapo wakati huu mwakani, utamkumbatia mwana. Akasema, La!
Bwana wangu, wewe mtu wa Mungu, usiniambie mimi mjakazi wako uongo. Yule
mwanamke akachukua mimba, akazaa mtoto mume wakati uo huo mwakani, kama Elisha
alivyomwambia.”
· Mwanamke
aitwaye Thabita au Dorkasi – Alijulikana sana kwa matendo yake ya ukarimu
na utoaji, alitoa muda wake mwingi na nguvu zake akifanya kazi za mikono kwa
kufuma ili kuwasaidia masikini na kuwavika wajane kiasi kwamba hata alipokufa
msiba wake uliwagusa wengi na Mungu alifanya Muujiza wa kumfufua kupitia Petro
Matendo 9:36-39
“Na mwanafunzi mmoja alikuwako Yafa, jina lake
Tabitha, tafsiri yake ni Dorkasi (yaani paa); mwanamke huyu alikuwa amejaa
matendo mema na sadaka alizozitoa. Ikawa siku zile akaugua, akafa; hata
walipokwisha kumwosha, wakamweka orofani. Na kwa kuwa mji wa Lida ulikuwa
karibu na Yafa, nao wanafunzi wamesikia ya kwamba Petro yuko huko, wakatuma
watu wawili kwake, kumsihi na kusema, Usikawie kuja kwetu. Petro akaondoka
akafuatana nao. Alipofika, wakampeleka juu orofani wajane wote wakasimama
karibu naye, wakilia na kumwonyesha zile kanzu na nguo alizozishona Dorkasi wakati
ule alipokuwa pamoja nao.”
· Mariam
Magdalene, Yoana na Suzana - Wanatajwa na wanawake wengine kuwa
walimtumikia Mungu kwa mali zao, unapoyachunguza maandiko utaweza kubaini ni
kama huduma hii ya utoaji japokuwa inatuhusu wote lakini imetajwa katiika
maandiko mara nyingi ikionyesha kuwa ni wanawake ndio waliongoza katika swala
zima la kumtolea Mungu kwa hiyo wanawake ni watoaji wazuri sana kuliko wanaume
katika ibada na utumishi
Luka 8:1-3. “Ikawa baada ya hayo alikuwa akizunguka-zunguka katika
miji na vijiji akihubiri na kuitangaza habari njema ya ufalme wa Mungu; na wale
Thenashara walikuwa pamoja naye, na wanawake kadha wa kadha ambao walikuwa na
pepo wabaya na magonjwa wakaponywa; nao ni Mariamu aitwaye Magdalene aliyetokwa
na pepo saba, na Yoana mkewe Kuza, wakili wake Herode, na Susana, na wengine
wengi, waliokuwa wakimhudumia kwa mali zao.”
Wanawake ni waombaji – Ingawa neno la Mungu linatoa wito kwa kila
mtu wa Mungu kuwa na tabia ya kuomba, na wanaume wengi katika maandiko walikuwa
waombaji, hata hivyo wako wanawake ambao wanaonekana kuwa walikuwa na rekodi ya
kuomba na maombi yao kuwa na matokeo makubwa sana, Neno la Mungu linaonyesha
kuwa zamani nyakati za Biblia wanawake walitumiwa kama viongozi na watu wenye
ujuzi wa kuomboleza wakati kunapotokea majanga na huzuni au hata misiba,
wanawake waliitwa kuiongoza jamii katika maombolezo, hii ni kwa sanabu wao
walikuwa na ujuzi mkubwa wa kuomboleza wakiwa na uwezo mkubwa wa kuinua sauti
kulia na kuimba na kusababisha maombolezo yaliyogusa mioyo, aidha waliongoza
familia nzima au taifa au mji mzima kuonyesha majonzi wakati wa vifo majanga na
hukumu ya Mungu, au wakati majanga yanaikaribia jamii pia walifundisha binti
zao na watu wengine jinsi ya kulia na kuomboleza wakati wa hali ngumu,
Maombolezo haya yakielekezwa katika mfumo wa kimaombi yanaweza kuleta matokeo
makubwa katika jamii, maombi ya wanawake kadhaa katika maandiko yalisababisha
matokeo
Yeremia 9:17-19 “Bwana wa majeshi asema
hivi, Fikirini ninyi, mkawaite wanawake waombolezao, ili waje; mkatume na
kuwaita wanawake wenye ustadi, ili waje; na wafanye haraka na kutuombolezea,
ili macho yetu yachuruzike machozi, na kope zetu zibubujike maji. Maana sauti
ya maombolezo imesikiwa toka Sayuni, Jinsi tulivyotekwa! tulivyofadhaika sana!
Kwa sababu tumeiacha nchi, kwa kuwa wameangusha makao yetu.”
· Hana - alipitia
ugumu wa kupata mtoto lakini kwa vile alikuwa mwombaji Mungu alimjibu kwa kumpa
nabii Samuel ambaye alitokea kuwa Baraka kubwa sana kwa Israel, ni katika
wakati wa Samuel Taifa lili imarika na kuwa na uamsho mkubwa wa kifalme kuanzia
Sauli mpaka Daudi; Baraka hizi zililijia taifa kwa sababu ya maombi ya Hana.
1Samuel 1:10-11
“Naye huyo mwanamke alikuwa na uchungu rohoni
mwake, akamwomba Bwana akalia sana. Akaweka nadhiri, akasema, Ee Bwana wa
majeshi, ikiwa wewe utaliangalia teso la mjakazi wako, na kunikumbuka, wala
usinisahau mimi mjakazi wako, na kunipa mimi mjakazi wako mtoto mume, ndipo
mimi nitakapompa Bwana huyo mtoto siku zote za maisha yake, wala wembe
hautamfikilia kichwani kamwe.”
· Anna
Binti Fanuel – Mwanamke wa mfano wa kuigwa ambaye inaonekana alikuwa mwombaji
kuliko waombaji wote waliopata kuorodhesha katika maandiko ana alikuwa
mjane na pia alikuwa mtu mwenye umri
mkubwa lakini hata hivyo maandiko yanaonyesha kuwa alikuwa mwenye uwezo mkubwa
katika kufunga na kudumu katika maombi uwezo wake katika kuomba
unatudhihirishia ya kuwa wanawake wanauwezo mkubwa sana kushiriki katika maombi
na kusababisha matokeo, Anna Binti Fanuel
alimjua Yesu Kristo wazi wazi baada ya kuzaliwa kwake na alipowasili
Yerusalem Hekaluni aliwatolea watu habari zake.
Luka 2:36-38 “Palikuwa na nabii mke, jina lake Ana, binti Fanueli, wa
kabila ya Asheri, na umri wake ulikuwa miaka mingi, alikuwa amekaa na mume
miaka saba baada ya uanawali wake. Naye ni mjane wa miaka themanini na minne;
haondoki katika hekalu, ila huabudu usiku na mchana kwa kufunga na kuomba. Huyu
alitokea saa ile ile akamshukuru Mungu, na wote waliokuwa wakiutarajia ukombozi
katika Yerusalemu akawatolea habari zake.”
Wanawake ni walimu wazuri wa neno la Mungu – Maandiko yanaonyesha
wazi kuwa wanawake wakiwa wacha Mungu, na wakiwa na ujuzi wa maandiko maana
yake wana uwezo mkubwa sana wa kuipitisha imani hiyo kwa wengine kwa
kuwafundisha na hata kuhubiri injili wanawake wamekuwa waalimu wa watoto wengi
makanisani, na nyumbani pia, lakini pia
wanaweza kutumiwa kuimarisha wanawake wachanga katika maswala ya malezi na
kusimamia nyumba zao vizuri, Biblia inaonyesha ujuzi wao wa kufudisha na
kuhubiri katika namna mbalimbali
· Wanaweza
kuwafunza wengine namna ya kulea na kuzihudumia ndoa zao – Tito 2:3-5 “Vivyo hivyo na wazee wa kike wawe na mwenendo wa
utakatifu; wasiwe wasingiziaji, wasiwe wenye kutumia mvinyo nyingi, bali
wafundishao mema; ili wawatie wanawake vijana akili, wawapende waume zao, na
kuwapenda watoto wao; na kuwa wenye kiasi, kuwa safi, kufanya kazi nyumbani
mwao, kuwa wema, kuwatii waume zao wenyewe; ili neno la Mungu lisitukanwe.”
· Wanaweza
kuwaelekeza wengine na kuwafundisha kukaa katika imani kwa usahihi – Matendo
18:24-26 “Basi Myahudi mmoja, jina lake Apolo,
mzalia wa Iskanderia, mtu wa elimu, akafika Efeso; naye alikuwa hodari katika
maandiko. Mtu huyo alikuwa amefundishwa njia ya Bwana; na kwa kuwa roho yake
ilikuwa ikimwaka, alianza kunena na kufundisha kwa usahihi habari za Yesu; naye
alijua ubatizo wa Yohana tu. Akaanza kunena kwa ujasiri katika sinagogi; hata
Prisila na Akila walipomsikia wakamchukua kwao, wakamweleza njia ya Bwana kwa
usahihi zaidi.”
· Wanaweza
kutumiwa katika kushuhudia na kuhubiri habari njema – Yohana 4:28-39 “Basi yule mwanamke akauacha mtungi wake, akaenda zake
mjini, akawaambia watu, Njoni, mtazame mtu aliyeniambia mambo yote
niliyoyatenda. Je! Haimkini huyu kuwa ndiye Kristo?Basi wakatoka mjini,
wakamwendea. Huko nyuma wanafunzi wakamsihi wakisema, Rabi, ule.Akawaambia,
Mimi ninacho chakula msichokijua ninyi.Basi wanafunzi wake wakasemezana, Je!
Mtu amemletea chakula? Yesu akawaambia, Chakula changu ndicho hiki, niyatende
mapenzi yake aliyenipeleka, nikaimalize kazi yake. Hamsemi ninyi, Bado miezi
minne, ndipo yaja mavuno? Tazama, mimi nawaambieni, Inueni macho yenu myatazame
mashamba, ya kuwa yamekwisha kuwa meupe, tayari kwa mavuno. Naye avunaye
hupokea mshahara, na kukusanya matunda kwa uzima wa milele, ili yeye apandaye
na yeye avunaye wapate kufurahi pamoja. Kwa maana hapo neno hilo huwa kweli,
Mmoja hupanda akavuna mwingine. Mimi naliwatuma myavune yale msiyoyataabikia;
wengine walitaabika, nanyi mmeingia katika taabu yao. Na katika mji ule
Wasamaria wengi walimwamini kwa sababu ya neno la yule mwanamke, aliyeshuhudia
kwamba, Aliniambia mambo yote niliyoyatenda.”
Mathayo 28:5-7.
“Malaika akajibu, akawaambia wale wanawake,
Msiogope ninyi; kwa maana najua ya kuwa mnamtafuta Yesu aliyesulibiwa. Hayupo
hapa; kwani amefufuka kama alivyosema. Njoni, mpatazame mahali alipolazwa.Nanyi
nendeni upesi, mkawaambie wanafunzi wake, Amefufuka katika wafu. Tazama,
awatangulia kwenda Galilaya; ndiko mtakakomwona. Haya, nimekwisha waambia.”
· Wanaweza
kutumiwa kuirithisha imani na ujuzi wa neno la Mungu kwa watoto wao – 2Timotheo
1:4-6 “Nami natamani sana kukuona, nikiyakumbuka
machozi yako, ili nijae furaha; nikiikumbuka imani uliyo nayo isiyo na unafiki,
ambayo ilikaa kwanza katika bibi yako Loisi, na katika mama yako Eunike, nami
nasadiki wewe nawe unayo. Kwa sababu hiyo nakukumbusha, uichochee karama ya
Mungu, iliyo ndani yako kwa kuwekewa mikono yangu.”
Wanawake wanaweza kuwa viongozi na watenda kazi pamoja nasi - Wanawake
wanaweza kuwa viongozi katika kanisa na kuwa na mchango mkubwa kwa watu wengi,
nyakati za kanisa la Kwanza Fibi alitambuliwa na Paulo mtume kama moja ya
watumishi katika kanisa lililokuwako Kenrea na aliaminiwa na hata kutumiwa
kupeleka waraka mmojawapo wa Paulo huko, tunajua katika lugha ya Kiingereza
Fibi kuwa ni Mwanamke kwa sababu anatajwa kwa neno “She” badala ya “He”
aidha wanawake wanaweza kutumika kama viongozi wa makanisa ya nyumbani na
kadhalika katika huduma nyingine za kichungaji na kinabii.
· Fibi - Warumi
16:1-2 “Namkabidhi kwenu Fibi, ndugu yetu, aliye
mhudumu wa kanisa lililoko Kenkrea; kwamba mmpokee katika Bwana, kama
iwapasavyo watakatifu; mkamsaidie katika neno lo lote atakalohitaji kwenu; kwa
sababu yeye naye amekuwa msaidizi wa watu wengi, akanisaidia mimi pia.”
· Lidia - Matendo
16:14-15 “Mwanamke mmoja, jina lake Lidia, mwenye
kuuza rangi ya zambarau, mwenyeji wa Thiatira, mcha Mungu, akatusikiliza,
ambaye moyo wake ulifunguliwa na Bwana, ayatunze maneno yaliyonenwa na Paulo.
Hata alipokwisha kubatizwa, yeye na nyumba yake, akatusihi, akisema, Kama
mmeniona kuwa mwaminifu kwa Bwana, ingieni nyumbani mwangu mkakae.
Akatushurutisha.”
Wanawake wanaweza kuongoza sifa kwa asili – Maandiko yanaonyesha
kuwa wanawake pia ni viongozi hodari wa kusifu, Maandiko yanaonyesha kuwa nabii
mke Miriam aliongoza watu katika kumsifu Mungu
na kuimba wimbo wa ushindi mara baada ya Israel kuvuka bahari ya shamu,
na pia tunamuona Deborah akiongoza sifa wakati wa waamuzi baada ya ushindi dhidi wakanaani, akliwa na
Baraka na Hana baada ya kujaliwa kuzaa mtoto Samuel alitunga shairi zuri sana
la kumsifu Mungu, Na Mariam baada ya kupewa habari na malaika kuwa atamzaa
mwokozi wa ulimwengu aliimba sahairi la aina yake, hawa ndio wanawake wanne
wanaotajwa katika Biblia wakijihusisha na kumsifu Mungu na waliomwimbia Bwana na kuonyesha kuwa wanawake
wanaweza kufanya huduma ya kuimba sifa na kuiongoza
· Miriam -
Kutoka 15:20-21 “Na Miriamu, nabii mke, ndugu yake
Haruni, akatwaa tari mkononi mwake; wanawake wakatoka wote wakaenda nyuma yake,
wenye matari na kucheza. Miriamu akawaitikia, Mwimbieni BWANA, kwa maana
ametukuka sana; Farasi na mpanda farasi amewatupa baharini.”
· Debora –
Waamuzi 5 1-5 “Ndipo Debora, na Baraka mwana wa
Abinoamu, wakaimba siku ile, wakisema; Kwa sababu wakuu walitangulia katika
Israeli, Kwa sababu watu walijitoa nafsi zao kwa hiari yao, Mhimidini Bwana. Sikieni,
enyi wafalme; tegeni masikio, enyi wakuu; Mimi, naam mimi, nitamwimbia Bwana;
Nitamhimidi Bwana, Mungu wa Israeli. Bwana, ulipotoka katika Seiri, Ulipokwenda
vitani kutoka mashamba ya Edomu, Nchi ilitetema, mbingu nazo zikadondoza maji,
Naam, mawingu yakadondoza maji. Milima ikayeyuka mbele za uso wa Bwana, Naam
hata Sinai ule mbele za uso wa Bwana, Mungu wa Israeli.”
· Hanna –
1Samuel 2:1-10 “Naye Hana akaomba, akasema, Moyo
wangu wamshangilia Bwana, Pembe yangu imetukuka katika Bwana, Kinywa changu
kimepanuka juu ya adui zangu; Kwa kuwa naufurahia wokovu wako; Hakuna aliye
mtakatifu kama Bwana; Kwa maana hakuna ye yote ila wewe, Wala hakuna mwamba
kama Mungu wetu. Msizidi kunena kwa kutakabari hivyo; Majivuno yasitoke
vinywani mwenu; Kwa kuwa Bwana ni Mungu wa maarifa, Na matendo hupimwa na yeye
kwa mizani. Pinde zao mashujaa zimevunjika, Na hao waliojikwaa wamefungiwa
nguvu. Walioshiba wamejikodisha ili kupata chakula, Na hao waliokuwa na njaa
wamepata raha. Naam, huyo aliyekua tasa amezaa watoto saba, Na yeye aliye na
wana wengi amedhoofika. Bwana huua, naye hufanya kuwa hai; Hushusha hata
kuzimu, tena huleta juu. Bwana hufukarisha mtu, naye hutajirisha; Hushusha
chini, tena huinua juu. Humwinua mnyonge kutoka mavumbini, Humpandisha mhitaji
kutoka jaani, Ili awaketishe pamoja na wakuu, Wakakirithi kiti cha enzi cha
utukufu; Kwa maana nguzo za dunia zina Bwana, Naye ameuweka ulimwengu juu
yake.Yeye atailinda miguu ya watakatifu wake; Bali waovu watanyamazishwa
gizani, Maana kwa nguvu hakuna atakayeshinda; Washindanao na Bwana watapondwa
kabisa; Toka mbinguni yeye atawapigia radi; Bwana ataihukumu miisho ya dunia;
Naye atampa mfalme wake nguvu, Na kuitukuza pembe ya masihi wake.”
·
Mariamu mama
yake Yesu – Luka 2:46-45 “ Mariamu akasema, Moyo wangu wamwadhimisha Bwana,Na roho
yangu imemfurahia Mungu, Mwokozi wangu; Kwa kuwa ameutazama Unyonge wa mjakazi
wake. Kwa maana, tazama, tokea sasa Vizazi vyote wataniita mbarikiwa;Kwa kuwa
Mwenye nguvu amenitendea makuu, Na jina lake ni takatifu.Na rehema zake hudumu
vizazi hata vizazi Kwa hao wanaomcha.Amefanya nguvu kwa mkono wake;
Amewatawanya walio na kiburi katika mawazo ya mioyo yao; Amewaangusha wakuu
katika viti vyao vya enzi; Na wanyonge amewakweza. Wenye njaa amewashibisha
mema, Na wenye mali amewaondoa mikono mitupu. Amemsaidia Israeli, mtumishi
wake; Ili kukumbuka rehema zake;Kama alivyowaambia baba zetu, Ibrahimu na uzao
wake hata milele.”
Wanawake wanaweza kufanya kazi kubwa mbalimbali katika mwili wa Kristo
– Mungu anaweza kuwatumiwa wanawake kwa karama mbalimbali, na kutoa pepo,
anaweza kuwatumia kuhubiri, kufundisha kufungua makanisa, kushuhudia lakini pia
wanawake wanaweza kuifanya kazi ya Mungu kwa bidi; Paulo mtume anawasalimia
watendakazi kadhaa katika waraka wake kwa Warumi huku akiwataja wanawake ambao
walikuwa na bidii na wenye kujitahidi sana katika kazi ya Mungu.
· Warumi
16:6 -12 “Nisalimieni Mariamu, aliyejitaabisha sana
kwa ajili yenu. Nisalimieni Androniko na Yunia, jamaa zangu, waliofungwa pamoja
nami, ambao ni maarufu miongoni mwa mitume; nao walikuwa katika Kristo kabla
yangu. Nisalimieni Ampliato, mpenzi wangu katika Bwana. Nisalimieni Urbano,
mtenda kazi pamoja nami katika Kristo, na Stakisi, mpenzi wangu. Nisalimieni Apele,
mwenye kukubaliwa katika Kristo. Nisalimieni watu wa nyumbani mwa Aristobulo.
Nisalimieni Herodioni, jamaa yangu. Nisalimieni watu wa nyumbani mwa Narkiso,
walio katika Bwana. Nisalimieni Trifaina na Trifosa, wenye bidii katika Bwana.
Nisalimieni Persisi, mpenzi aliyejitahidi sana katika Bwana.”
Mungu hajamuokoa mwanamke ili awe
mtazamaji katika ufalme wa Mungu, wanawake ni washiriki wenza katika kusudi na
mpango wote wa Mungu, kila mwanamke anapaswa kuwajibika na kuongeza bidii
katika kumtumikia Mungu, wanawake wanapaswa kujiamini, wanapaswa kuwa na
ujasiri, wanapaswa kutumia vipawa na karama walizopewa na Mungu na wanapaswa
kukumbuka kuwa Mungu hana upendeleo, tumia kila ulichonacho na utumishi wote na
huduma zote zinazoelekezwa katika kanisa fanya huku ukiijenga famlia yako,
kulihudumia kanisa na kutangaza habari njema.
Kanisa lenye wanawake waombaji ni
kanisa lenye nguvu, Kanisa lenye wanawake wanaolijua neno ni kanisa imara,
Kanisa lenye wanwake wanaohubiri ni kanisa linalokua kwa kasi, kanisa lenye
wanawake wanaofundisha vijana ni kanisa lenye watu wenye nidhamu, kanisa lenye
wanawake wahuburi ni kanisa linalosambaa, kanisa lenye wanawake wanaotoa ni kanisa linaloweza kuisukuma kazi ya Mungu
na kuwatunza watumishi vema, kanisa lenye wanawake watakatifu ni kanisa lenye
ushuhuda wenye nguvu, tunataka kanisa letu liwe na wanawake imara sana katika
imani
Rev. Innocent Samuel Kamote

