Daniel 9:3-4 “Nikamwelekezea
Bwana Mungu uso wangu, ili kutaka kwa maombi, na dua, pamoja na kufunga, na
kuvaa nguo za magunia na majivu. Nikamwomba Bwana, Mungu wangu, nikaungama,
nikasema, Ee Bwana, Mungu mkuu, mwenye kutisha, ashikaye maagano na rehema kwao
wampendao, na kuzishika amri zake;”
Utangulizi:
Ni Tarehe 15/03/2025 Mida ya Mchana nikiwa kijiji
cha Loiborsoit A, Wilayani Simanjiro, Mkoani Manyara, tunaelekea kwenye Harusi
ya kimila ya kijana wa rafiki yetu, katika jamii ya kimasai, njiani ninaongozana
na kijana wa kimasai Morani (Nyangulo).
Na kijana wa zamani (Kuriyanga) namuuliza harusi hii ya kimila itafungwa
saa ngapi ananiambia itafungwa saa nne za usiku, namuuliza ni kwanini
haikufungwa kanisani? Kijana wa kimaasai akaniambia, Kanisani? Hapana sisi
tunaogopa kuvunja maagano, Hatuwezi kwenda kufunga ndoa ya kanisani kwa sababu
tutaapishwa, tutamuahidi Mungu kuwa nitakuwa na mwanamke huyu tu na wengine
wote nitawaepuka, na sitawatamani wengine, jambo ambalo ni la uongo na linaweza
kuleta laana kwetu, au mwanamke anaweza kunisumbua nikabadili mawazo, kwa nini
nimdanganye Mungu na kuapa au kujifunga katika agano ambalo ukweli sitaweza
kulitimiza kwa hiyo nafikiri ndoa hii ya kimila isiyo na kiapo chochote ni
nzuri na nafuu kuliko zile ndoa zenu za kanisani!
Hili lilinipa kutafakari sana na kunipa swali kubwa
la kujiuliza Je wakristo wa leo kweli wanashika maagano? Kwanini ndoa nyingi
sana leo zinavunjika tena ndoa za kilokole je wanajua gharama za kuvunja maagano?
Je wanahofu na wanajua kuwa Mungu hushika maagano? Je wanajua kuwa kuvunja
agano huleta laana na madhara makubwa sana? Je hivi wanajua kuwa ndoa ni agano?
Leo hii ndoa nyingi sana zinavunjika hususani za watu wanaojulikana kama waliokoka.
Hakimu mmoja alisema siku hizi watu wakija mahakamani wakiwa na madai kuwa
wanataka kuachana tunauliza tu ninyi ni wakristo? Wanajibu ndio swali la pili
ni wa madhehebu gani? Wakitujibu kuwa ni ya Kipentekoste basi haraka sana
tunaandika talaka kwa sababu wao ndio ambao kesi zao tumezichoka na ndio
wanaoongoza kwa kuvunja ndoa! Na ndio
wanaoongoza leo kwa kubadili mwelekeo na kuvunja ndoa, kwa hiyo
hatuzicheleweshi alisema hakimu huyo! Kwa kweli watu waliookoka hawaogopi
kuvunja maagano wala hawajui hatari yake na kama wanajua basi hawajajua madhara
makubwa ya kuvunja maagano! Kwa sababu hiyo leo tuarudi tena katika maandiko
kujifunza tena kwa kina na mapana na marefu kuhusiana na agano la ndoa na
tutaliangalia somo hili kwa kuzingatia vipengele vinne vifuatavyo:-
·
Tofauti ya Agano na maswala mengine.
·
Madhara ya kuvunja agano.
·
Mifano ya watu waliovunja agano na kupata
madhara.
·
Mambo ya kufanya unapokuwa umevunja agano.
Tofauti ya Agano na mambo mengine.
Kabla hatujafanya Uchambuzi wa kina kuhusu maana ya
neno Agano ni muhimu kwetu tukayachambua mambo mengine muhimu yanayofanana na
agano ambayo yatatusaidia kulielewa vema neno Agano ambalo ni la muhimu Zaidi
katika ujumbe wetu huu wa leo!
1. Agano ni tofauti na “Mkataba”. A contract.
Mkataba ni mapatano ya
kimaneno au kimaandishi yanayohusisha pande mbili katika kufikia jambo fulani
Bila kumuhusisha Mungu; Mkataba unaweza kuwa mkataba wa mauzo, kazi, ajira na
kadhalika Kwa kawaida Mtu anapovunja mkataba yule atakayeuvunja kabla ya wakati
huwajibika kulipa fidia.
2. Agano ni tofauti na ”Nadhiri”. A ”Vow” or ” an Oath”
Tofauti na mkataba Nadhiri ni
ahadi anayoitoa mtu akijifunga kwa Mungu huku akitarajia Mungu amfanyie yeye
kitu ili yeye atimize kile alichoahidi Mfano
Waamuzi 11:29-31. ”Ndipo roho
ya Bwana ikamjilia juu yake Yeftha, naye akapita katika Gileadi na Manase,
akapita na katika Mispa ya Gileadi, na kutoka hapo Mispa ya Gileadi akapita
kuwaendea wana wa Amoni. Naye Yeftha akamwekea Bwana nadhiri, akasema, Kwamba
wewe utawatia wana wa Amoni mkononi mwangu kweli, ndipo itakuwa ya kwamba, kile
kitakachotoka katika milango ya nyumba yangu kunilaki, hapo nitakaporudi na
amani kutoka kwa hao wana wa Amoni, kitu hicho kitakuwa ni cha Bwana, nami
nitakisongeza kiwe sadaka ya kuteketezwa.”
1Samuel 1:10-11 ”Naye huyo mwanamke alikuwa na uchungu rohoni mwake,
akamwomba Bwana akalia sana. Akaweka nadhiri, akasema, Ee Bwana wa majeshi,
ikiwa wewe utaliangalia teso la mjakazi wako, na kunikumbuka, wala usinisahau
mimi mjakazi wako, na kunipa mimi mjakazi wako mtoto mume, ndipo mimi
nitakapompa Bwana huyo mtoto siku zote za maisha yake, wala wembe hautamfikilia
kichwani kamwe. Ikawa, hapo alipodumu kuomba mbele za Bwana, Eli akamwangalia
kinywa chake.”
Hata hivyo maandiko yanashauri
kutokuweka nadhiri na kama mtu ataweka nadhiri anashauriwa kukumbuka kuiondoa, kutokuitendea
kazi nadhiri kunaweza kushababisha madhara makubwa kwani Mungu anakumbuka
lakini wanadamu tunasahau, kuweka nadhiri na kushindwa kuiondoa ni Upumbavu kwa
mujibu wa maandiko ona:-
Muhubiri 5:4-6 ”Wewe ukimwekea Mungu nadhiri, usikawie kuiondoa; kwa kuwa
yeye hawi radhi na wapumbavu; basi, uiondoe hiyo uliyoiweka nadhiri. Ni
afadhali usiweke nadhiri, Kuliko kuiweka usiiondoe. Usikiache kinywa chako
kuukosesha mwili wako; wala usiseme mbele ya huyo malaika ya kwamba
umepitiliwa; kwani Mungu akukasirikie sauti yako, na kuiharibu kazi ya mikono
yako?”
Kwa mujibu wa andiko hili,
ukiweka nadhiri kisha ukakawia kuiondoa maana yake unafanya upumbavu, kwa hiyo
tunashauriwa kuiondoa, na tunaelezwa kuwa ni afahdali kutokuweka nadhiri,
kuliko kuiweka usiiondoe kwa kufanya hivyo kinywa chako kinahatarisha maisha
yako, na malaika ndio huwa wanakuwa ni mashahidi na wanaofuatilia nadhiri,
kutokuondoa nadhiri husababisha Mungu akukasirikie na sio hivyo tu analaani
kazi za mikono yako, kwa hiyo ndio kusema kuwa madhara mengine yanatokana na
vinywa vyetu wenyewe kwa kuahidi tusiyoweza kuyatekeleza kwa Mungu.
3. Agano ni tofauti na ”kiapo” an Oath
Hii ni ahadi anayojiapiza mtu
kwa Mungu au kwa mwenzake ili kuuthibitisha ukweli au uaminifu kuwa atafanya
yale aliyoahidi au anayoahidi kuyafanya kama kukabidhiwa madaraka, kwa kawaida
kutokutimiza kiapo ni dhambi na inaruhusu hukumu ya Mungu, wanadamu ni waongo
na ni wachache tu wanaoweza kusimamia yale wanayoyaahidi, Yesu alitahadharisha
sana kuhusu swala la kiapo akitutaka wanafunzi wake kuwa tusiape kabisa bali
aliagiza kuwa majibu yetu yawe ndio, ndio au Siyo, siyo.
Mathayo 5:33-37 ”Tena mmesikia watu wa kale walivyoambiwa, Usiape uongo,
ila mtimizie Bwana nyapo zako; lakini mimi nawaambia, Usiape kabisa; hata kwa
mbingu, kwa maana ndicho kiti cha enzi cha Mungu; wala kwa nchi, kwa maana
ndiyo pa kuwekea miguu yake; wala kwa Yerusalemu, kwa maana ndio mji wa Mfalme
mkuu. Wala usiape kwa kichwa chako, maana huwezi kufanya unywele mmoja kuwa
mweupe au mweusi. Bali maneno yenu yawe Ndiyo, ndiyo; Siyo, siyo; kwa kuwa
yazidiyo hayo yatoka kwa yule mwovu.”
Kwa nini Yesu aliagiza
tusiape? Kwa kuwa inagharimu hukumu mtu asipotimiza kiapo, Mungu ni wa kuheshimiwa sana mbingu ni
kiti chake cha enzi, inchi ni sehemu yake ya kuwekea miguu yake na Yerusalem ni
mji wa mfalme mkuu (masihi) wala kwa kichwa chako kwa sababu huwezo kuongeza au
kupunguza siku zako kwa msingi huo basi Yesu alituonya kuhusu kiapo na kututaka
kuwa wakweli.
Yakobo 5:12 ” Lakini
zaidi ya yote, ndugu zangu, msiape, wala kwa mbingu wala kwa nchi; wala kwa
kiapo kinginecho chote; bali ndiyo yenu na iwe ndiyo, na siyo yenu iwe siyo,
msije mkaangukia hukumu.”.
Kuapia/kiapo ndiko
kulikopelekea kifo cha Yohana mbatizaji kutokea Mathayo 14:6-10 ”Hata ilipofika sikukuu ya
kuzaliwa kwake Herode, binti Herodia alicheza mbele ya watu, akampendeza
Herode. Hata akaahidi kwa kiapo ya kwamba atampa lo lote atakaloliomba.Naye,
huku akichochewa na mamaye, akasema, Nipe hapa katika kombe kichwa cha Yohana Mbatizaji.
Naye mfalme akasikitika; lakini kwa ajili ya viapo vyake, na kwa ajili ya wale
walioketi chakulani pamoja naye, akaamuru apewe; akatuma mtu, akamkata kichwa
Yohana mle gerezani.”
Mungu pia huweza kuapa kwake
binafsi kwani hana mkubwa dhidi yake hivyo huweza kujiapia yeye Mwenyewe hii ni
ili athibitishe kwetu jinsi alivyo muaminifu
Waebrania 6:13-18 ”Maana
wanadamu huapa kwa yeye aliye mkuu kuliko wao; na kwao ukomo wa mashindano yote
ya maneno ni kiapo, kwa kuyathibitisha. Katika neno hilo Mungu, akitaka
kuwaonyesha zaidi sana warithio ile ahadi, jinsi mashauri yake yasivyoweza
kubadilika, alitia kiapo katikati; ili kwa vitu viwili visivyoweza kubadilika,
ambavyo katika hivyo Mungu hawezi kusema uongo, tupate faraja iliyo imara, sisi
tuliokimbilia kuyashika matumaini yale yawekwayo mbele yetu;”
Sasa basi Mungu anapoapa
kumuelekea mwanadamu kiapo hicho huitwa Agano pia. Na mwanadamu na mwanadamu
wanapoapiana mbele za Mungu au Mungu akiwa ni shahidi yao au huku wakimuhusisha
Mungu hilo huwa ni AGANO kama ilivyo kwa wanandoa wanapooana kanisani na
ikafanyika ibada ya kuwaunganisha kihalali basi hilo huitwa agano. ”Covenant” na likivunjwa lina madhara
makubwa kwa pande zote mbili na hususani yule aliyeanza kuvunja agano.
4.
Agano ni nini hasa
Neno agano ambalo kwa
kiingereza linajulikana kama Covenant katika lugha ya asili ya kiibrania
linajulikana kama ”Berit” ambalo
maana yake ni makubaliano yanayofanyika baina ya pande mbili huku Mungu akiwa
ni shahidi, Neno Berit pia
humaanisha fungamano la kudumu ambalo halikatiki, na linakatika kwa mtu mmoja
kufa ili mwenzake awe huru kwa hiyo kwa kiibrania neno Berit pia lilimaanisha ”to
Cut” yaani kukata au kukatika au kupasuliwa vipande viwili, kuchinjwa kwa
hiyo zamani watu walipofanya agano walichinja mnyama na damu ya mnyama huyo
ilimwagika, kisha mnyama alipasuliwa vipande viwili na wahusika walipaswa kupita
katikati ya mnyama huyo ili kwamba endapo upande mmoja usipotimiza agano hilo
utapata adhabu ya kifo sawa na kifo cha mnyama yule
Mwanzo 15:9-21 ”Akamwambia,
Unipatie ndama wa miaka mitatu, na mbuzi mke wa miaka mitatu, na kondoo mume wa
miaka mitatu, na hua, na mwana njiwa. Akampatia hao wote, akawapasua vipande
viwili, akaweka kila kipande kuelekea mwenzake, ila ndege hakuwapasua. Hata tai
walipotua juu ya mizoga Abramu akawafukuza. Na jua lilipokuwa likichwa usingizi
mzito ulimshika Abramu, hofu ya giza kuu ikamwangukia. BWANA akamwambia Abramu,
Ujue hakika ya kwamba uzao wako utakuwa mgeni katika nchi isiyo yake,
watawatumikia watu wale, nao watateswa muda wa miaka mia nne. Hata na taifa
lile, watakaowatumikia, nitawahukumu; baadaye watatoka na mali mengi. Lakini
wewe utakwenda kwa baba zako kwa amani, utazikwa katika uzee mwema. Na kizazi
cha nne kitarudi hapa, maana haujatimia uovu wa Waamori bado. Ikawa, jua
lilipokuchwa likawa giza, tazama, tanuru ya moshi na mwenge unaowaka ulipita
kati ya vile vipande vya nyama. Siku ile BWANA akafanya agano na Abramu,
akasema, Uzao wako nimewapa nchi hii, kutoka mto wa Misri mpaka huo mto mkubwa,
mto Frati, Mkeni, na Mkenizi, na Mkadmoni, na Mhiti, na Mperizi, na Mrefai, na
Mwamori, na Mkanaani, na Mgirgashi, na Myebusi.”
Katika maandiko hayo tunaona
Mungu akifanya agano na Abrahamu, agano la kumpa nchi ya Kanaani, hata hivyo ni
Mungu ndiye aliyepita katikati ya mnyama aliyeuawa na sio Abrahamu, hii
ilimaanisha kuwa Mungu alikuwa tayari hata kuyatoa maisha yake endapo
hangemtimizia Abrahamu ahadi yake hili lilikuwa ni agano, kama agano likivunjwa
mtu mmoja aliyevunja agano hilo anatakiwa kufa. Agano linapokuwa limefanyika
hata kama upande mmoja utakuwa ulifanya hila na ulikuwa hujazigundua hila hizo,
ukamuapia utapaswa kutimiza agano hilo na kama na kama utafanya vinginevyo
madhara makubwa sana yatakupata katika maisha yako hususani kifo na laana
nyinginezo!
Yoshua 9:1-27 ”Kisha ikawa
hapo wafalme wote waliokaa ng'ambo ya pili ya Yordani, hapo penye nchi ya
vilima, na katika Shefela, na katika upande wa pwani yote ya bahari kubwa
kuikabili Lebanoni, yaani, huyo Mhiti, na Mwamori, na Mkanaani, na Mperizi, na
Mhivi, na Myebusi, waliposikia habari ya mambo hayo; ndipo walipojikutanisha
pamoja wenyewe kwa wenyewe, ili kupigana na Yoshua, na hao Israeli, kwa nia
moja. Lakini wenyeji wa Gibeoni waliposikia habari ya hayo yote Yoshua
aliyokuwa amewatenda watu wa Yeriko, na wa Ai,
wao wakatenda kwa hila, nao wakaenda na kujifanya kama ndio wajumbe,
wakaenda na magunia makuukuu juu ya punda zao, na viriba vya mvinyo vilivyokuwa
vikuukuu vilivyoraruka-raruka, na kutiwa viraka; na viatu vilivyotoboka na
kushonwa-shonwa katika miguu yao, na mavao makuukuu waliyokuwa wanavaa; tena
mkate wote wa chakula chao ulikuwa umekauka na kuingia koga. Nao wakamwendea
Yoshua hata maragoni huko Gilgali, nao wakamwambia yeye na watu wa Israeli,
Sisi tumetoka nchi ya mbali sana; basi kwa hiyo fanyeni agano pamoja nasi. Basi
watu wa Israeli wakawaambia hao Wahivi, Labda mwakaa kati yetu; nasi tutawezaje
kufanya agano nanyi? Nao wakamwambia
Yoshua, Sisi tu watumishi wako. Yoshua akawauliza, Ninyi ni nani? Nanyi mwatoka
wapi? Nao wakamwambia, Sisi watumishi wako twatoka nchi iliyo mbali sana, kwa
sababu ya jina la Bwana, Mungu wako; kwa kuwa sisi tumesikia sifa zake, na
habari ya hayo yote aliyofanya huko Misri, na habari ya hayo yote aliyowatenda
wale wafalme wawili wa Waamori, waliokuwa huko ng'ambo ya pili ya Yordani,
maana huyo Sihoni, mfalme wa Heshboni, na Ogu, mfalme wa Bashani, aliyekuwa
huko Ashtarothi. Kisha wazee wetu, na wenyeji wote wa nchi yetu, walinena nasi
na kutuambia, Chukueni vyakula mkononi mwenu kwa ajili ya safari, mwende
mkawalaki watu hao, na kuwaambia, Sisi tu watumishi wenu; basi sasa fanyeni
agano nasi. Huu mkate wetu tuliutwaa ukali moto katika nyumba zetu, siku hiyo
tuliyotoka kuja kwenu, uwe chakula chetu; lakini sasa, tazama, umekauka, na
kuingia koga; na viriba vyetu hivi, tulivyovitia divai, vilikuwa ni vipya;
sasa, tazama, vimeraruka-raruka; na haya mavazi yetu na viatu vyetu vimekuwa
vikuukuu kwa vile tulivyokuja safari ya mbali sana. Basi hao watu wakatwaa
katika vyakula vyao, wala wasitake shauri kinywani mwa Bwana. Naye Yoshua
akafanya amani pamoja nao, na kufanya agano nao, ili kwamba waachwe hai; na
wakuu wa mkutano wakawaapia. Kisha ikawa, mwisho wa siku ya tatu baada ya
kufanya hilo agano nao, walisikia habari ya kuwa watu hao ni jirani zao, na ya
kwamba waliketi kati yao. Kisha wana wa Israeli walisafiri, wakaifikilia miji
ya watu hao siku ya tatu. Basi miji ya watu hao ilikuwa ni hii, Gibeoni, na
Kefira, na Beerothi, na Kiriath-yearimu. Wana wa Israeli hawakuwapiga, kwa
sababu wakuu wa mkutano walikuwa wamekwisha kuwaapia kwa Bwana, Mungu wa
Israeli. Nao mkutano wote wakawanung'unikia hao wakuu. Lakini wakuu wote
waliwaambia mkutano wote, Sisi tumewaapia kwa Bwana, Mungu wa Israeli; basi
sasa hatuwezi kuwagusa watu hawa. Tutawafanyia neno hili, kisha tutawaacha wawe
hai; hasira isije juu yetu, kwa ajili ya hicho kiapo tulichowaapia.Wakuu
waliwaambia, Waacheni wawe hai; basi wakawa wenye kupasua kuni, na wenye kuteka
maji, kwa ajili ya mkutano wote; vile vile kama hao wakuu walivyowaambia. Basi
Yoshua akawaita, akanena nao, na kuwaambia, Mbona ninyi mmetudanganya, huku
mkisema, Sisi tu mbali sana na ninyi; nanyi kumbe! Mwakaa kati yetu? Basi sasa
mmelaaniwa kisha hatakosekana kuwapo mtu wa kwenu aliye mtumwa, wenye kupasua
kuni, na wenye kuteka maji, kwa ajili ya nyumba ya Mungu wangu. Nao wakamjibu
Yoshua, na kusema, Ni kwa sababu ya sisi watumishi wako kuambiwa hakika, jinsi
huyo Bwana, Mungu wako alivyomwamuru mtumishi wake Musa kuwapa ninyi nchi hii
yote, na kuwaangamiza wenyeji wote wa nchi hii watoke mbele zenu; kwa sababu
hii tuliogopa mno kwa ajili ya uhai wetu kwa sababu yenu, nasi tumefanya neno
hili. Basi sasa, tazama, sisi tu mkononi mwako; basi kama uonavyo kuwa ni vyema
na haki kwako wewe kututenda, tutende vivyo. Naye akawafanyia hivyo, na kuwaokoa
na mkono wa wana wa Israeli, ili wasiwaue. Siku iyo hiyo Yoshua akawafanya kuwa
ni wenye kupasua kuni, na wenye kuteka maji, kwa ajili ya mkutano, na kwa ajili
ya madhabahu ya Bwana, hata siku hii ya leo, katika mahali hapo atakapopachagua.”
Israel walifanya agano na
Wagibeoni bila kujua kuwa wagibeoni waliishi Kanaani na kuwa waliwadanganya
Israel baadaye walipogundua waliwajibika kuwalinda kwa sababu waliapa kuwa na
amani nao na kama wangeliwaua ingewagharimu Israeli kufa au kupata madhara
kutoka kwa Mungu kwa sababu ya agano hilo, wakati fulani Sauli Mfalme wa Israel
aliuwa baadhi wa wagibeoni kinyume na agano hili na madhara makubwa
yaliipata Israel na familia yake hata
wakati wa utawala wa Daudi
2Samuel 21:1-9 ”Kulikuwa na
njaa siku za Daudi muda wa miaka mitatu, mwaka kwa mwaka; naye Daudi akautafuta
uso wa Bwana. Bwana akasema, Ni kwa ajili ya Sauli, na kwa nyumba yake yenye
damu, kwa kuwa aliwaua hao Wagibeoni. Ndipo mfalme akawaita Wagibeoni
akawaambia; (basi Wagibeoni si wa wana wa Israeli, ila ni wa masalio ya
Waamori; na wana wa Israeli walikuwa wamewaapia; lakini Sauli akatafuta kuwaua
katika juhudi yake kwa ajili ya wana wa Israeli na Yuda;) basi Daudi akawaambia
hao Wagibeoni, Niwatendee nini? Na kwa tendo gani nifanye upatanisho, mpate kuubariki
urithi wa Bwana? Na hao Wagibeoni wakamwambia, Si jambo la fedha wala dhahabu
lililo kati ya sisi na Sauli, au nyumba yake; wala si juu yetu kumwua mtu ye
yote katika Israeli. Akasema Mtakayoyanena, ndiyo nitakayowatendea ninyi.
Wakamwambia mfalme, Yule mtu aliyetupoteza, na kutufanyia shauri la kutuharibu,
tusikae katika mipaka yo yote ya Israeli, basi, na tutolewe watu saba katika
wanawe, nasi tutawatundika mbele za Bwana katika Gibeoni, katika mlima wa
Bwana. Mfalme akasema, Nitawatoa. Lakini mfalme akamwachilia Mefiboshethi,
mwana wa Yonathani, mwana wa Sauli, kwa ajili ya kiapo cha Bwana kilichokuwa
kati yao, yaani, kati ya Daudi na Yonathani, mwana wa Sauli. Ila mfalme
akawatwaa hao wana wawili wa Rispa, binti Aya, aliomzalia Sauli, Armoni na
Mefiboshethi; na wana watano wa Merabu binti Sauli, aliomzalia Adrieli, mwana
wa Barzilai, Mmeholathi; akawatia mikononi mwa Wagibeoni, nao wakawatundika
mlimani mbele za Bwana, nao wakaangamia wote saba pamoja; wakauawa siku za
mavuno, za kwanza, mwanzo wa mavuno ya shayiri.”
Kwa hiyo wote tumeona na
kufahamu na kutambua kuhusu agano sasa kwa bahati mbaya au njema ndoa zote za
watu wa Mungu huangukia katika sifa za kuwa na agano, sio patano, sio mkataba,
wala sio nadhiri, kwa sababu hiyo mwanandoa awaye yote anapomtendea mwenzake
mambo ya hiyana anavunja agano, mfano kama mwanamke anamnyima mumewe tendo la
ndoa pasipo sababu za msingi analivunja agano na kwa sababu hiyo anapaswa kufa
na hatouawa na mwanadamu bali atauawa na Mungu mwenyewe, au anaweza kupata
madhara makubwa na yakamgharimu sana na mwanamke akimuacha mkewe au watu hao
wakitalikiana wanalivunja agano na yule ambaye ndiye chanzo au sababu ya
mgogoro huo kifo kinamuhusu na yeye aliye sababu za mwanzoni za kupelekea agano
kuharibika atatangulia kufa ni kwa sababu kama hizo Neno la Mungu linatahadharisha
wanandoa kutokufanyiana mambo ya hiyana kinyume na kile kilichoahidiwa katika
maandiko ona :-
Malaki 2:13-16 ”Tena mnatenda
haya nayo; mnaifunikiza madhabahu ya Bwana kwa machozi, kwa kulia na kwa
kuugua, hata asiiangalie tena hiyo dhabihu, wala kuitakabali mikononi mwenu na
kuiridhia. Lakini ninyi mwasema, Ni kwa sababu gani? Ni kwa sababu Bwana
amekuwa shahidi kati ya wewe na mke wa ujana wako, uliyemtenda mambo ya hiana,
angawa yeye ni mwenzako, na mke wa agano lako. Hakuna mtu mmoja aliyetenda
hivi, ambaye alikuwa na ufahamu kidogo. Au je! Kuna mtu mmoja atafutaye mzao
mwenye kumcha Mungu? Kwa hiyo jihadharini roho zenu; mtu awaye yote asimtende
mke wa ujana wake mambo ya hiana. Maana mimi nakuchukia kuachana, asema Bwana,
Mungu wa Israeli; naye aifunikizaye nguo yake kwa udhalimu namchukia, asema
Bwana wa majeshi; basi jihadharini roho zenu, msije mkatenda kwa hiana.”
1Wakorintho 7:3-5 ”Mume na
ampe mkewe haki yake, na vivyo hivyo mke na ampe mumewe haki yake. Mke hana
amri juu ya mwili wake, bali mumewe; vivyo hivyo mume hana amri juu ya mwili
wake, bali mkewe. Msinyimane isipokuwa mmepatana kwa muda, ili mpate faragha
kwa kusali; mkajiane tena, Shetani asije akawajaribu kwa kutokuwa na kiasi
kwenu.”
Waebrania 13:4 ”Ndoa na
iheshimiwe na watu wote, na malazi yawe safi; kwa maana waasherati na wazinzi
Mungu atawahukumia adhabu.”
Watu wengi hawafahamu kuwa
kunyimana tendo la ndoa ni kuvunja agano la ndoa, katika vitu ambavyo
huwaunganisha wanandoa na kuwafanya waache kila kitu kwa wazazi wao ni pamoja
na tendo la ndoa, lakini kwa bahati mbaya watu wengi hunyimana tendo la ndoa
huku wakilitumia tendo hilo kama fimbo ya kuadhibiana na kusahau kuwa waliapa
mbele za Mungu na mashahidi wake na wakiwa hawajui kama ni kosa na ni uvunjifu
wa ukiukwaji wa haki za agano, aidha kama wana ndoa hao pia watafanya uasherati
na zinaa Mungu atawahukumia adhabu kwa sababu wanalivunja agano na kusababisha
madhara makubwa sio kwa familia na ndoa pekee lakini pia kwa ardhi na inchi na
kufanya mambo kuwa magumu sana. Kwa ujumla kuvunja agano lolote lile liwe la
kimila au linalomuhusisha Mungu kiroho ni jambo baya sana na lina madhara
makubwa! Na mara nyingi sana wanadamu
walipovunja agano la Mungu Mungu aliilaani ardhi kwaajili yao ili kusababisha
madhara juu yao na kizazi chao
Mwanzo 3:17-19 ”Akamwambia
Adamu, Kwa kuwa umeisikiliza sauti ya mke wako, ukala matunda ya mti ambao
nalikuagiza, nikisema, Usiyale; ardhi imelaaniwa kwa ajili yako; kwa uchungu
utakula mazao yake siku zote za maisha yako; michongoma na miiba itakuzalia,
nawe utakula mboga za kondeni; kwa jasho la uso wako utakula chakula, hata
utakapoirudia ardhi, ambayo katika hiyo ulitwaliwa; kwa maana u mavumbi wewe,
nawe mavumbini utarudi.”
Mwanzo 4:10-14 ”Akasema,
Umefanya nini? Sauti ya damu ya ndugu yako inanililia kutoka katika ardhi. Basi
sasa, umelaaniwa wewe katika ardhi, iliyofumbua kinywa chake ipokee damu ya
ndugu yako kwa mkono wako; utakapoilima ardhi haitakupa mazao yake; utakuwa
mtoro na mtu asiye na kikao duniani. Kaini akamwambia BWANA, Adhabu yangu
imenikulia kubwa, haichukuliki. Tazama, umenifukuza leo katika uso wa ardhi,
nitasitirika mbali na uso wako, nami nitakuwa mtoro na mtu asiye na kikao
duniani; hata itakuwa kila anionaye ataniua. ”
Unaweza kuona kuwa mara nyingi
sana Mwanadamu alipokosea na kutenda dhambi ya kuvunja agano au kuua Mungu
aliilaani ardhi hii ni kwa sababu kadhaa za muhimu za kiroho na kimaandiko,
kuvunja agano au kuua na kumwaga damu juu ya nchi na dhambi nyinginezo zote
huathiri chanzo cha asili ya mwanadamu
Mwanadamu alitoka katika
mavumbi ya ardhi kwa hiyo uko uhusiano wa karibu sana kati ya ardhi na
mwanadamu, ardhi ni mama wa mwanadamu na madhara ya dhambi hukimbilia katika
ardhi ambayo ni chanzo cha uhai wako, ardhi inakuwa ngumu kukunufaisha, ardhi
inakukataa na kusababisha ugumu wa maisha na kutokufanikiwa na zaidi sana
kupunguza uwezekano wa kuishi siku nyingi, ardhi inapolaaniwa kwaajili yako
maana yake unaongezewa ugumu wa maisha na kupunguziwa siku zako za kuishi
Mwanzo 2:7 ”BWANA Mungu
akamfanya mtu kwa mavumbi ya ardhi, akampulizia puani pumzi ya uhai; mtu akawa
nafsi hai.”
Mungu alimpa mwanadamu ardhi,
ardhi ndio eneo la utawala wa mwanadamu, ni katika ardhi ndiko kunakotkea
mafanikio yetu yote ya kimwili, utajiri wa kila kitu uko ardhini kwa hiyo
mwanadamu alitakiwa kuitawala ardhi na kuitunza na kuilima kwa hiyo mwanadamu anapotenda
dhambi ikiwa ni pamoja na kuvunja agano laana hukimbilia katika ardhi ili
kuifanya kazi ya mwanadamu kuwa ngumu sana Zaburi
115:16 ” Mbingu ni mbingu za Bwana, Bali nchi
amewapa wanadamu.”
Mwanzo 1:28 ”Mungu
akawabarikia, Mungu akawaambia, Zaeni, mkaongezeke, mkaijaze nchi, na
kuitiisha; mkatawale samaki wa baharini, na ndege wa angani, na kila kiumbe
chenye uhai kiendacho juu ya nchi. Mungu akasema, Tazama, nimewapa kila mche
utoao mbegu, ulio juu ya uso wa nchi yote pia, na kila mti, ambao matunda yake
yana mbegu; vitakuwa ndivyo chakula chenu; na chakula cha kila mnyama wa nchi,
na cha kila ndege wa angani, na cha kila kitu kitambaacho juu ya nchi, chenye
uhai; majani yote ya miche, ndiyo chakula chenu; ikawa hivyo.”
Ardhi ndiyominayobeba baraka
za wanadamu na ndiyo inayobeba laana za wanadamu, wanadamu wanapofanya dhambi
na dhuluma na kuvunja maagano yaani zinaa nchi ndiyo inayoomboleza kwa hiyo
madhara ya dhambi hubebwa na ardhi au nchi ile
Yeremia 23:10 ” Maana nchi imejaa wazinzi; kwa sababu ya
kuapa nchi inaomboleza; malisho ya nyikani yamekauka; mwenendo wao ni mbaya, na
nguvu zao si za haki.”
Kuvunja maagano kumesababisha
laana na maisha magumu sana katika jamii na kutokufanikiwa na kutokupata
ufumbuzi kwa sababu aliyekosewa na Mungu mwenyewe aliye shahidi wa maagano
yanayovunjwa kila iitwapo leo, karibu laana zote zinazowapata wanadamu
zinaungamanishwa na ardhi
Kumbukumbu 28:15-20 ”Lakini
itakuwa usipotaka kuisikiza sauti ya Bwana, Mungu wako, usiyaangalie kufanya
maagizo yake yote na amri zake, nikuagizazo hivi leo, ndipo zitakapokujia laana
hizi zote na kukupata. Utalaaniwa mjini, utalaaniwa na mashambani. Litalaaniwa
kapu lako na chombo chako cha kukandia. Utalaaniwa uzao wa tumbo lako, na uzao
wa nchi yako, maongeo ya ng'ombe wako, na wadogo wa kondoo zako. Utalaaniwa
uingiapo, utalaaniwa na utokapo, Bwana atakuletea laana na mashaka, na
kukemewa, katika yote utakayotia mkono wako kuyafanya, hata uangamie na kupotea
kwa upesi; kwa ule uovu wa matendo yako, uliyoniacha kwayo.”
Madhara ya kuvunja agano
Kuvunja agano kuna madhara makubwa sana na kunasababisha laana na hukumu ya Mungu
ambayo kilele chake ni kifo na kama utaishi utaishi maisha ya taabu sana, na
kula mkate wa shida, wakati mwingine madhara ya kuvunja agano yanaweza kuathiri
sio mtu mmoja tu bali na jamii yake ni ukweli ulio wazi kuwa hata watu wa Musa,
walionywa kuwa laana ya Mungu ingembatana na wale wasiotii na wenye kulivunja
agano la Mungu kwa hiyo kuna madhara makubwa sana na nilimuelewa kijana yule wa
kimaasai aliposema sisi tunaogopa kuvunja agano! Hapa yako madhara
yanayoambatana na kuvunjwa kwa agano, huku masaini kila changamoto inapotokea
wamasai hukimbilia kuchinja mwana kondoo kwaajili ya kuondoa laana katika
ardhi, hata hivyo sisi tunayo damu ya Yesu ambayo huvunja na kuharibu laana
zote na kutunenea mema kama damu ya Habili.
1. Kuvunja
agano kunakaribisha hukumu ya Mungu
Kumbukumbu
28:15-67 “Lakini itakuwa usipotaka kuisikiza sauti
ya Bwana, Mungu wako, usiyaangalie kufanya maagizo yake yote na amri zake,
nikuagizazo hivi leo, ndipo zitakapokujia laana hizi zote na kukupata. Utalaaniwa
mjini, utalaaniwa na mashambani. Litalaaniwa kapu lako na chombo chako cha
kukandia. Utalaaniwa uzao wa tumbo lako, na uzao wa nchi yako, maongeo ya
ng'ombe wako, na wadogo wa kondoo zako. Utalaaniwa uingiapo, utalaaniwa na
utokapo, Bwana atakuletea laana na mashaka, na kukemewa, katika yote utakayotia
mkono wako kuyafanya, hata uangamie na kupotea kwa upesi; kwa ule uovu wa matendo
yako, uliyoniacha kwayo. Bwana atakuambatanisha na tauni, hata atakapokwisha
kukuondoa katika nchi uingiayo kwa kuimiliki. Bwana atakupiga kwa kifua kikuu,
na kwa homa, na kwa kuwashwa, na kwa hari ya moto, na kwa upanga, na kwa
ukaufu, na kwa koga; navyo vitakufukuza hata uangamie. Na mbingu zako zilizo
juu ya kichwa chako zitakuwa shaba, na nchi iliyo chini yako itakuwa chuma. Bwana
atafanya mvua ya nchi yako iwe vumbi na mchanga; itakujilia juu yako kutoka
mbinguni hata uangamie. Bwana atakufanya upigwe mbele ya adui zako; utawatokea
juu yao kwa njia moja, lakini utakimbia mbele yao kwa njia saba; nawe utatupwa
huko na huko katika falme zote za duniani. Na mzoga wako utakuwa chakula cha
ndege wote wa angani, na wanyama wote wa duniani, pasiwe na mtu wa kuwafukuza. Bwana
atakupiga kwa majipu ya Misri, na kwa bawasiri, na kwa pele, na kwa kujikuna,
ambayo hupati kupoa. Bwana atakupiga kwa wazimu, na kwa upofu, na kwa bumbuazi
la moyoni; utakwenda kwa kupapasa-papasa mchana, kama apapasavyo kipofu gizani,
wala hufanikiwi katika njia zako; nawe sikuzote utaonewa na kutekwa nyara, wala
hapatakuwa na mtu wa kukuokoa. Utaposa mke na mume mwingine atalala naye;
utajenga nyumba usiikae; utapanda mizabibu usitumie matunda yake. Ng'ombe wako
atachinjwa mbele ya macho yako, usile nyama yake; utanyang'anywa punda wako
mbele ya uso wako kwa jeuri, usirudishiwe; kondoo zako watapewa adui zako,
usipate mtu wa kukuokoa. Wanao na binti zako litapewa taifa lingine, na macho
yako yataangalia, na kuzimia kwa kuwatamani mchana kutwa; wala hapatakuwa na
kitu katika uwezo wa mkono wako. Matunda ya nchi yako, na taabu yako yote,
vitaliwa na taifa usilolijua; utaonewa tu, na kupondwa chini daima; hata uwe
mwenye wazimu kwa yaonwayo na macho yako, utakayoyaona. Bwana atakupiga magoti
na miguu kwa jipu lililo zito, usilopata kupozwa, tokea wayo wa mguu mpaka
utosi wa kichwa. Bwana atakupeleka wewe, na mfalme wako utakayemweka juu yako,
kwa taifa usilolijua wewe wala baba zako; nawe huko utatumikia miungu mingine
ya miti na mawe. Nawe utakuwa ushangao, na mithali, na dharau, kati ya mataifa
yote huko atakakokuongoza Bwana. Mbegu nyingi utazichukua nje shambani, lakini
utavuna haba, kwa kuwa nzige watazila. Utapanda mizabibu na kuitengeza, wala
hutakunywa katika divai yake, wala kuichuma kwani italiwa na mabuu. Utakuwa na
mizeituni katika mipaka yako yote usijipake mafuta yake; kwa kuwa mzeituni wako
utapukutika. Utazaa wana na binti, lakini hawatakuwa wako wewe; kwa sababu
watakwenda utumwani. Miti yako yote, na mazao ya nchi yako, nzige watakuwa
nayo. Mgeni aliye kati yako atazidi kupaa juu yako; nawe utazidi kushuka chini.
Yeye atakukopesha, wala wewe usimkopeshe; yeye atakuwa ni kichwa, wewe utakuwa
mkia. Na laana hizi zote zitakujilia juu yako, zitakuandama na kukupata, hata uangamizwe,
kwa kuwa hukuisikiza sauti ya Bwana, Mungu wako, kushika maagizo yake na amri
zake alizokuagiza; nazo zitakuwa juu yako kwa ishara na ajabu, na juu ya uzao
wako milele; kwa kuwa hukumtumikia Bwana, Mungu wako, kwa furaha na moyo wa
kushukuru, kwa ajili ya ule wingi wa vitu vyote; kwa hiyo utawatumikia adui
zako atakaowaleta Bwana juu yako, kwa njaa, na kwa kiu, na kwa uchi, na kwa
uhitaji wa vitu vyote; naye atakuvika kongwa la chuma shingoni mwako, hata
atakapokwisha kukuangamiza. Bwana atakuletea taifa juu yako kutoka mbali,
kutoka ncha ya dunia, kama arukavyo tai; taifa usiloufahamu ulimi wake; taifa
lenye uso mkali, ambalo haliangalii uso wa mzee, wala halipendelei kijana; naye
atakula uzao wa ng'ombe wako wa mifugo, na uzao wa nchi yako mpaka
utakapokwisha kuangamizwa; wala hatakuachia nafaka, wala divai, wala mafuta,
wala maongeo ya ng'ombe wako, wala wana-kondoo wako, hata atakapokwisha
kukuangamiza. Naye atakuhusuru katika malango yako yote, hata kuta zako ndefu,
zenye maboma, ulizokuwa ukiziamini, zishuke, katika nchi yako yote kila upande;
naye atakuhusuru katika malango yako yote kila upande, katika nchi yako yote
aliyokupa Bwana, Mungu wako. Nawe utakula uzao wa tumbo lako mwenyewe, nyama ya
wana wako na binti zako aliokupa Bwana, Mungu wako; katika mazingirwa na katika
mkazo utakaokazwa na adui zako. Mtu mume kati yenu aliye mwororo na laini sana,
jicho lake litakuwa ovu juu ya nduguye, na juu ya mke wa kifuani mwake, na juu
ya masalio ya wanawe waliosalia naye; hata asitake wao mmojawapo apewe katika
nyama ya wanawe atakaowala, kwa kuwa hana kitu kilichomsalia kwake; katika
mazingirwa na mkazo utakaokazwa na adui yako katika malango yako yote. Mwanamke
kati yenu aliye mwororo na laini, ambaye hangehatirisha kuweka wayo wa mguu
wake nchi kwa umalidadi na ulaini, jicho lake huyu litakuwa ovu juu ya mume wa
kifuani mwake, na juu ya mwanawe, na juu ya binti yake, na juu ya mchanga wake
atokaye katikati ya miguu yake, na juu ya wanawe atakaowazaa; kwa kuwa atawala
kwa siri, kwa uhitaji wa vitu vyote; katika mazingirwa na mkazo utakaokazwa na
adui yako katika malango yako. Kama hutaki kutunza kufanya maneno yote ya
torati hii yaliyoandikwa katika kitabu hiki, upate kulicha jina hili la fahari na
utisho, Bwana, MUNGU WAKO; ndipo atakapofanya Bwana mapigo yako yawe ya ajabu,
na mapigo ya uzao wako, mapigo makubwa kwa kweli, ya kudumu sana, na magonjwa
mazito ya kudumu sana. Naye atakurejezea maradhi yote ya Misri juu yako
uliyokuwa ukiyaogopa, nayo yataambatana nawe. Tena kila ugonjwa, na kila pigo
yasiyoandikwa katika kitabu cha torati hii, atakutia nayo Bwana juu yako, hata
utakapokwisha kuangamizwa. Nanyi mtasalia wachache kwa hesabu, ninyi mliokuwa
mfano wa nyota za mbinguni kwa wingi; kwa kuwa hukuisikiza sauti ya Bwana,
Mungu wako.Tena itakuwa, kama vile alivyokuwa akifurahi Bwana juu yenu kwa
kuwatendea mema na kuwafanya kuwa wengi, ndivyo atakavyofurahi Bwana juu yenu
kwa kuwapoteza na kuwaangamiza; nanyi mtanyakuliwa katika hiyo nchi mwingiayo
kuimiliki.Bwana atakutawanya katika mataifa yote, tokea ncha hii ya dunia hata
ncha hii ya dunia; nawe huko utatumikia miungu mingine usiyoijua wewe wala baba
zako, nayo ni miti na mawe. Wala katika mataifa hayo hutapata raha iwayo yote,
wala hutakuwa na kituo cha wayo wa mguu wako; lakini Bwana atakupa huko moyo wa
kutetema, na macho ya kuzimia, na roho ya kudhoofika; na uzima wako utakuwa na
wasiwasi mbele yako; nawe utakuwa na woga usiku na mchana, wala hutaamini kamwe
maisha yako; asubuhi utasema, Laiti ingekuwa jioni! Na jioni utasema, Laiti
ingekuwa asubuhi! Kwa kicho cha moyo wako utakavyokucha, na kuona kwa macho
yako utakavyoona.”
2. Kuvunja
agano kunakufanya utengwe na Mungu
Kuvunja agano kunasababisha mtu utengwe
kiroho na Mungu, jambo litakalopelekea upoteze Baraka na ulinzi wa Mungu
Yeremia
31:31-33 “Angalia, siku zinakuja, asema Bwana,
nitakapofanya agano jipya na nyumba ya Israeli, na nyumba ya Yuda. Si kwa mfano
wa agano lile nililolifanya na baba zao, katika siku ile nilipowashika mkono,
ili kuwatoa katika nchi ya Misri; ambalo agano langu hilo walilivunja, ingawa
nalikuwa mume kwao, asema Bwana. Bali agano hili ndilo nitakalofanya na nyumba
ya Israeli, baada ya siku zile, asema Bwana; Nitatia sheria yangu ndani yao, na
katika mioyo yao nitaiandika; nami nitakuwa Mungu wao, nao watakuwa watu wangu.”
Katika kifungu hiki cha maandiko Mungu
anakumbuika na kusikitika kuwa Israel walilivunja agano agano lake na kwa
sababu hiyo hii ilisababisha watengwe na Mungu na kupelekwa utumwani huko
Babeli, Hakuna jambo baya duniani kama kutengwa na uso wa Mungu, Ulinzi wake
unaondoka na unakabiliwa na uonevu na kila atakayekuona atakuua tu
Mwanzo
4:13-14 “Kaini akamwambia BWANA, Adhabu yangu
imenikulia kubwa, haichukuliki.Tazama, umenifukuza leo katika uso wa ardhi,
nitasitirika mbali na uso wako, nami nitakuwa mtoro na mtu asiye na kikao
duniani; hata itakuwa kila anionaye ataniua.”
3. Kuvunja
agano husababisha laana na adhabu kali
Kwa ujumla kuvunja aano kunasababisha
madhara makubwa sana ikiwemo kupoteza Baraka, kupelekwa utumwani, kutengwa
kiroho na Mungu, hukumu mbaa, kwa ujumla kuna adhabu kali sana zinazoambatana
na laana na madhara mbalimbali
Walawi
26:14-16 “Mtoe huyo aliyeapiza nje ya marago; na
wale wote waliomsikia na waweke mikono yao kichwani mwake, kisha mkutano wote
na wamwue kwa kumpiga kwa mawe. Nawe nena na wana wa Israeli na kuwaambia, Mtu
awaye yote atakayemlaani Mungu wake atachukua dhambi yake. Na yeye
atakayelikufuru jina la BWANA hakika atauawa; mkutano wote watamwua kwa kumpiga
kwa mawe; kama ni mgeni, kama ni mzalia, hapo atakapolikufuru jina la BWANA
atauawa.”
4. Kuvunja
agano kunasababisha Magonjwa, laana na utasa na kushindwa vita
Yeremia
34:18-20 “Na watu hao waliolivunja agano langu,
wasioyatimiza maneno ya agano lile, walilolifanya mbele zangu, wakati ule
walipomkata ndama vipande viwili, wakapita katikati ya vipande vile; wakuu wa
Yuda, na wakuu wa Yerusalemu, matowashi, na makuhani, na watu wote wa nchi,
waliopita katikati ya vipande vile vya huyo ndama; mimi nitawatia katika mikono
ya adui zao, na katika mikono ya watu wale wanaowatafuta roho zao, na mizoga
yao itakuwa ni chakula cha ndege za mbinguni, na cha wanyama wakali wa nchi.”
Agano la Mungu linaposhikwa kwa uaminifu
husababisha Baraka mbalimbali ikiwepo, Baraka ya uzao, kubarikiwa mashambani,
kupewa ushindi vitani, kuwa na nguvu dhidi ya maadui zako, na mengineyo mengi,
lakini linapovunjwa hali huwa tofauti, utatiwa mikononi mwa adui zako,
utaonewa, utapata utasa, utakosa uzao, hali itakuwa mbaya kila eneo la maisha
yako, maswala ya maisha yako mengi na milango ya Baraka mingi itafungwa
Mungu ataachilia laana za kila aina kwa
wale wanaokosa uaminifu kwa agano walilolifanya mbele zake, kumbuka kuwa
inaweza kuchukua muda mrefu sana kuona hali hiyo kwa sababu Mungu sio mwepesi
wa hasira lakini hata hivyo hawezi kuvumilia hata mwisho na kukuacha bila madhara
endapo umekuwa mstari wa mbele kuvunja agano lake, na kama ulikuwa hujagundua
mpaka utakapokuja kugundua utakuwa umeshateseka sana
Mifano ya watu waliovunja agano na kupata
madhara
Kuvunja agano ni kosa kubwa sana linaloharibu haki
na utakatifu wa Mungu, ni udhalilishaji mkubwa sana kwa upande wa Mungu ambaye
anatazamia, umakini mkubwa wa uaminifu katika makubaliano baina yetu na yeye, Maandiko
yanaonyesha kuwa kuna madhara makubwa sana yanayowapata watu wanapovunja
maagano na kusababisha madhara na changamoto kubwa na za kudumu, Mungu ni kweli
ni mwingi wa huruma na rehema na neema lakini vile vile ni Mungu wa haki,
hawezi kuachilia dhuluma itawale akiwa yeye ni mwenye haki.
Mwanzo 18:25 “Hasha
usifanye hivyo, ukamwue mwenye haki pamoja na mwovu, mwenye haki awe kama
mwovu. Hasha; Mhukumu ulimwengu wote asitende haki?”
1. Adam
na Eva – walikuwa na agano
na Mungu ambalo lilistawishwa katika bustani ya Edeni ambapo Mungu aliwataka
wasile kutoka katika mti wa ujuzi wa mema na mabaya lakini katika hali
isiyokuwa ya kawaida Adam na Eva walikula tunda walilokatazwa na haraka sana
kuvunjwa kwa agano lile kulipelekea kuweko kwa madhara makubwa sana, kifo cha
kiroho, kufukuzwa kutoka katika uwepo wa Mungu na Bustani ya Edeni, kuzaa kwa
uchungu, kula kwa jasho, kuzaliwa kwa michongoma, kulaaniwa kwa ardhi, na kifo haya yakawa ni madhara ya kudumu kutoka
kwa Adamu na hata uzao wake hata leo
Mwanzo
3:16-19 “Akamwambia mwanamke, Hakika nitakuzidishia
uchungu wako, na kuzaa kwako; kwa utungu utazaa watoto; na tamaa yako itakuwa
kwa mumeo, naye atakutawala. Akamwambia Adamu, Kwa kuwa umeisikiliza sauti ya
mke wako, ukala matunda ya mti ambao nalikuagiza, nikisema, Usiyale; ardhi
imelaaniwa kwa ajili yako; kwa uchungu utakula mazao yake siku zote za maisha
yako; michongoma na miiba itakuzalia, nawe utakula mboga za kondeni; kwa jasho
la uso wako utakula chakula, hata utakapoirudia ardhi, ambayo katika hiyo
ulitwaliwa; kwa maana u mavumbi wewe, nawe mavumbini utarudi.”
2. Wana
wa Israel – Walipewa agano
na Mungu kupitia Musa mtumishi wake katika mlima wa Sinai, lakini mara kwa mara
wana wa Israel walilivunja agano hilo kwa kuabudu miungu jambo ambalo mara kwa
mara lilisababisha mapigo na kuchelewa kuingia katika nchi ya kanaani kwa miaka
40
Kutoka
32:31-35 “Musa akarejea kwa BWANA akasema, Aa! Watu
hawa wametenda dhambi kuu wamejifanyia miungu ya dhahabu. Walakini sasa, ikiwa
utawasamehe dhambi yao na kama sivyo, unifute, nakusihi, katika kitabu chako
ulichoandika. BWANA akamwambia Musa, Mtu ye yote aliyenitenda dhambi ndiye
nitakayemfuta katika kitabu changu. Basi sasa uende ukawaongoze watu hawa mpaka
mahali pale ambapo nimekwambia habari zake; tazama, malaika wangu
atakutangulia; pamoja na hayo siku nitakayowajilia nitawapatiliza kwa ajili ya
dhambi yao. BWANA akawapiga hao watu, kwa walivyoifanya ile ndama, ambayo
Haruni aliifanya.”
3. Mfalme
Sauli kwa kuwaua wagibeoni – Aliweza
kusababisha madhara ya kuuawa kwa watoto wake saba, kwa sababu aliwaua Wagibeoni na kusahau kuwa Israel walikuwa
wamefanya nao agano na Mungu ni Mungu ashikaye maagano
2Samuel
1-9 “Kulikuwa na njaa siku za Daudi muda wa miaka
mitatu, mwaka kwa mwaka; naye Daudi akautafuta uso wa Bwana. Bwana akasema, Ni
kwa ajili ya Sauli, na kwa nyumba yake yenye damu, kwa kuwa aliwaua hao
Wagibeoni. Ndipo mfalme akawaita Wagibeoni akawaambia; (basi Wagibeoni si wa
wana wa Israeli, ila ni wa masalio ya Waamori; na wana wa Israeli walikuwa
wamewaapia; lakini Sauli akatafuta kuwaua katika juhudi yake kwa ajili ya wana
wa Israeli na Yuda;) basi Daudi akawaambia hao Wagibeoni, Niwatendee nini? Na
kwa tendo gani nifanye upatanisho, mpate kuubariki urithi wa Bwana? Na hao Wagibeoni
wakamwambia, Si jambo la fedha wala dhahabu lililo kati ya sisi na Sauli, au
nyumba yake; wala si juu yetu kumwua mtu ye yote katika Israeli. Akasema
Mtakayoyanena, ndiyo nitakayowatendea ninyi. Wakamwambia mfalme, Yule mtu
aliyetupoteza, na kutufanyia shauri la kutuharibu, tusikae katika mipaka yo
yote ya Israeli, basi, na tutolewe watu saba katika wanawe, nasi tutawatundika
mbele za Bwana katika Gibeoni, katika mlima wa Bwana. Mfalme akasema,
Nitawatoa. Lakini mfalme akamwachilia Mefiboshethi, mwana wa Yonathani, mwana
wa Sauli, kwa ajili ya kiapo cha Bwana kilichokuwa kati yao, yaani, kati ya
Daudi na Yonathani, mwana wa Sauli. Ila mfalme akawatwaa hao wana wawili wa
Rispa, binti Aya, aliomzalia Sauli, Armoni na Mefiboshethi; na wana watano wa
Merabu binti Sauli, aliomzalia Adrieli, mwana wa Barzilai, Mmeholathi; akawatia
mikononi mwa Wagibeoni, nao wakawatundika mlimani mbele za Bwana, nao
wakaangamia wote saba pamoja; wakauawa siku za mavuno, za kwanza, mwanzo wa
mavuno ya shayiri.”
Kwa ujumla kuvunja maagano kuna madhara makubwa
sana na kunaleta laana juu ya nchi, maisha na mwenendo mzima wa watu, hapa ni
maagano ya namna zote likiwepo agano la ndoa, linapovunjwa agano la aina yoyote
ambalo kwalo Mungu ni shahidi ni ukweli ulio wazi kuwa kunakuwa na madhara
makubwa sana kwa kuvunjwa kwa agano hilo kwa sababu Mungu ni Mungu ashikaye
maagano na alijulikana hivyo na watakatifu waliotutangulia. watakatifu waliotutangulia walimfahamu Mungu jinsi alivyo
muaminifu katika kushika maagano
walipoomba, walimkumbusha Mungu sifa yake hii jinsi alivyo muaminifu
katika kushika maagano walipoomba walimkumbusha Mungu ahadi alizojifunga kwao
au kwa Baba zao Ibrahimu, Isaka na Yakobo, kuhusu Agano na rehema zake hii
inapandisha sana imani kujua kuwa Mungu wetu ni Mungu muaminifu si muongo,
Hesabu 23:19. “Mungu
si mtu, aseme uongo; Wala si mwanadamu, ajute; Iwapo amesema, hatalitenda?
Iwapo amenena, hatalifikiliza? ”
Wanadamu ni waongo lakini Mungu si muongo wala si
mwanadamu hata ajute Yeye akinena hutenda na ni muaminifu toka kizazi hata
kizazi Fadhili zake zinadumu hata milele wakati mnapoweka Agano na mwenzi wako
au na unapofanya agano lolote lile na yeye akawa ni shahidi basi fahamu ya kuwa
agano hilo ukilivunja Mungu anakasirishwa na anapatiliza na madhara yake ni
kifo.
Mambo ya kufanya unapokuwa umevunja agano
Rafiki yangu katika jamii ya kimasai aliniambia
kuwa katika ardhi ya kimasai hakuna jambo linaogopewa kama laana, anasema
katika jamii yetu hata mtu akiumizwa kiasi cha kutoa damu, wazee lazima
watachinja kondoo kwaajili ya upatanishi na kuzuia laana, na vile vile kama mtu
amevunja agano basi ni lazima achinje kondoo ili laana iwe mbali naye na pia
ardhi iweze kubarikiwa! Wamasai wakati wote wanahakikisha kuwa ikiwezekana
achinjwe kondoo au mbuzi kuhakikisha kuwa wao na inchi yao inakuwa salama, kwa
bahati nzuri sisi sasa sisi tunayo Damu ya Yesu Kristo ambayo imemwagika
msalabani na ina nguvu na uwezo wa kutuokoa na laana na dhambi kama tutamwendea
yeye kwa toba na kufanya mapinduzi makubwa ya kugeuzwa nia zetu na kuiitia damu
ya Yesu yenye nguvu ya kutakasa kutuondolea changamoto zinazotukabili.
Waebrania 9:11-15 “Lakini
Kristo akiisha kuja, aliye kuhani mkuu wa mambo mema yatakayokuwapo, kwa hema
iliyo kubwa na kamilifu zaidi, isiyofanyika kwa mikono, maana yake, isiyo ya
ulimwengu huu, wala si kwa damu ya mbuzi na ndama, bali kwa damu yake mwenyewe
aliingia mara moja tu katika Patakatifu, akiisha kupata ukombozi wa milele. Kwa
maana, ikiwa damu ya mbuzi na mafahali na majivu ya ndama ya ng'ombe
waliyonyunyiziwa wenye uchafu hutakasa hata kuusafisha mwili; basi si zaidi
damu yake Kristo, ambaye kwamba kwa Roho wa milele alijitoa nafsi yake kwa
Mungu kuwa sadaka isiyo na mawaa, itawasafisha dhamiri zenu na matendo mafu,
mpate kumwabudu Mungu aliye hai? Na kwa sababu hii ni mjumbe wa agano jipya,
ili, mauti ikiisha kufanyika kwa kukomboa makosa yaliyokuwa chini ya agano la
kwanza, hao walioitwa waipokee ahadi ya urithi wa milele”
Waebrania 10:1-10 “Basi
torati, kwa kuwa ni kivuli cha mema yatakayokuwa, wala si sura yenyewe ya mambo
hayo, kwa dhabihu zile zile wanazozitoa kila mwaka daima, haiwezi wakati wo
wote kuwakamilisha wakaribiao. Kama ndivyo, je! Dhabihu hazingekoma kutolewa;
kwa maana waabuduo, wakiisha kusafishwa mara moja, wasingejiona tena kuwa na
dhambi? Lakini katika dhabihu hizo liko kumbukumbu la dhambi kila mwaka. Maana
haiwezekani damu ya mafahali na mbuzi kuondoa dhambi. Kwa hiyo ajapo ulimwenguni,
asema, Dhabihu na toleo hukutaka, Lakini mwili uliniwekea tayari; Sadaka za
kuteketezwa na sadaka za dhambi hukupendezwa nazo; Ndipo niliposema, Tazama,
nimekuja (katika gombo la chuo nimeandikiwa) Niyafanye mapenzi yako, Mungu.
Hapo juu asemapo, Dhabihu na matoleo na sadaka za kuteketezwa na hizo za dhambi
hukuzitaka, wala hukupendezwa nazo (zitolewazo kama ilivyoamuru torati), ndipo
aliposema, Tazama, nimekuja niyafanye mapenzi yako. Aondoa la kwanza, ili
kusudi alisimamishe la pili. Katika mapenzi hayo mmepata utakaso, kwa kutolewa
mwili wa Yesu Kristo mara moja tu.”
Iwapo umejiingiza katika swala zima la
kuharibu maagano haya ndiyo yakupasayo kufanya
1. Tambua
kuwa umeharibu agano – hatua
ya kwanza ni lazima utambue ya kuwa umeharibu umevunja agano na kukubali kuwa
umefanya upumbavu kwa kuvunja maagano ya Bwana, hii itajumuisha kujitathimini
na kujitambua na kuanza kujutia huku ukimwambia Mungu dhambi ya kuvunja agano
1Wafalme
19:9-10. “Akafika kunako pango, akalala ndani yake.
Na tazama, neno la Bwana likamjia, naye akamwambia, Unafanya nini hapa, Eliya?
Akasema, Nimeona wivu mwingi kwa ajili ya Bwana Mungu wa majeshi; kwa kuwa wana
wa Israeli wameyaacha maagano yako, na kuzivunja madhabahu zako, na kuwaua
manabii wako kwa upanga; nami nimesalia, mimi peke yangu; nao wanitafuta roho
yangu, waiondoe.”
Hosea
6:6-7 “Maana nataka fadhili wala si sadaka; na
kumjua Mungu kuliko sadaka za kuteketezwa. Lakini wao wamelivunja hilo agano
kama Adamu; huko wamenitenda mambo ya hiana.”
Yeremia
11:10 “Wameyarudia maovu ya baba zao, waliokataa
kusikia maneno yangu; wamewafuata miungu mingine na kuwatumikia; nyumba ya
Israeli, na nyumba ya Yuda, wameyavunja maagano yangu niliyoyafanya na baba
zao. Basi, Bwana asema hivi, Tazama, nitaleta mabaya juu yao, ambayo hawataweza
kuyakimbia; nao watanililia, walakini sitawasikiliza.”
Daniel
9:3-11 “Nikamwelekezea Bwana Mungu uso wangu, ili
kutaka kwa maombi, na dua, pamoja na kufunga, na kuvaa nguo za magunia na
majivu. Nikamwomba Bwana, Mungu wangu, nikaungama, nikasema, Ee Bwana, Mungu
mkuu, mwenye kutisha, ashikaye maagano na rehema kwao wampendao, na kuzishika
amri zake; tumefanya dhambi, tumefanya ukaidi, tumetenda maovu, tumeasi, naam,
hata kwa kuyaacha maagizo yako na hukumu zako; wala hatukuwasikiliza watumishi
wako, manabii, ambao kwa jina lako walisema na wafalme wetu, na wakuu wetu, na
baba zetu, na watu wote wa nchi. Ee Bwana, haki ina wewe, lakini kwetu sisi
kuna haya ya uso, kama hivi leo; kwa watu wa Yuda, na kwa wenyeji wa
Yerusalemu, na kwa Israeli wote, walio karibu na hao walio mbali, katika nchi
zote ulikowafukuza, kwa sababu ya makosa yao waliyokukosa.Ee Bwana, kwetu sisi
kuna haya ya uso, kwa wafalme wetu, na wakuu wetu, na baba zetu, kwa sababu
tumekutenda dhambi. Rehema na msamaha ni kwa Bwana Mungu wetu, ingawa
tumemwasi; wala hatukuitii sauti ya Bwana, Mungu wetu, kwa kwenda katika sheria
zake, alizoziweka mbele yetu kwa kinywa cha watumishi wake, manabii. Naam,
Israeli wote wameihalifu sheria yako, kwa kugeuka upande, wasiisikilize sauti
yako; basi kwa hiyo laana imemwagwa juu yetu, na uapo ule ulioandikwa katika
sheria ya Musa, mtumishi wa Mungu; kwa sababu tumemtenda dhambi.”
Baada ya kuwa umetafakari ni maagano gani
umeyavunja na kujutia na kusikitika sasa unaweza kufanya toba.
2. Tubu
– kutubu maana yake
ni kuadhimia au kudhamiria kugeuka, acha matendo yote yanayohusisha kuvunja
maagano ahadi na maagizo yote ya Mungu, omba neema na rehema na msamaha kwa
Mungu, badilika fanya mageuzi makubwa na rudi katika njia iliyo sahihi kwa
Mungu
Matendo
3:18-20 “Lakini mambo yale aliyohubiri Mungu tangu
zamani kwa kinywa cha manabii wake wote, ya kwamba Kristo wake atateswa,
ameyatimiza hivyo. Tubuni basi, mrejee, ili dhambi zenu zifutwe, zipate kuja
nyakati za kuburudishwa kwa kuwako kwake Bwana; apate kumtuma Kristo Yesu
mliyewekewa tangu zamani;”
Warumi
12:2 “Wala msiifuatishe namna ya dunia hii; bali
mgeuzwe kwa kufanywa upya nia zenu, mpate kujua hakika mapenzi ya Mungu yaliyo
mema, ya kumpendeza, na ukamilifu.”
3. Amini
katika msamaha wa Mungu – Lazima
umwendee yeye kwa imani, ukiamini katika msamaha wake, omba rehema, mweleze
Mungu kile ambacho umeharibu, amini katika neno lake ambalo limesema ya kuwa
tukiziungama dhambi zetu yeye atatusamehe
1Yohana
1:9 “Tukiziungama dhambi zetu, Yeye ni mwaminifu na
wa haki hata atuondolee dhambi zetu, na kutusafisha na udhalimu wote.”
4. Chukua
hatua stahiki - Kama uliondoka katika ndoa yako rudi,
ulimwacha mkeo rejea kwa mkeo, ulimuacha mumeo rejea kwa mumeo, acha wanawake
wote na wanaume wote ambao wanaisumbua ndoa yako, acha uasherati, acha zinaa,
achana na michepuko, vunja uhusiano wako wa kimapenzi na wanawake au wanaume
wote ambao wewe hujafanya nao agano, enenda katimize kile ambacho ulikuwa
umekiapia au umefanya agano nacho
Ezra
10:1-5 “Basi hapo Ezra alipokuwa akiomba na
kuungama, akilia, na kujiangusha kifudifudi mbele ya nyumba ya Mungu,
wakamkusanyikia katika Israeli wote kusanyiko kubwa sana la wanaume, na
wanawake, na watoto; maana watu hao walikuwa wakilia sana. Hata Shekania, mwana
wa Yehieli, mmoja wa wana wa Elamu, akajibu, akamwambia Ezra, Sisi tumemkosa
Mungu wetu, nasi tumeoa wanawake wageni wa watu wa nchi hizi; lakini kungaliko
tumaini kwa Israeli katika jambo hili. Haya basi! Na tufanye agano na Mungu
wetu, kuachana na wake zetu, na wale waliozaliwa nao, tukilifuata shauri la
bwana wangu, na shauri la hao wanaoitetemekea amri ya Mungu wetu; mambo haya na
yatendeke kwa kuifuata torati. Inuka; maana shughuli hii yakuhusu wewe; na sisi
tu pamoja nawe; uwe na moyo mkuu, ukaitende. Ndipo Ezra akaondoka, akawaapisha
wakuu wa makuhani, na Walawi, na Israeli wote, ya kwamba watafanya kama hayo.
Basi wakaapa.”
5. Fanya
agano jipya na Mungu – Baada ya maamuzi magumu sasa unaweza
kumwambia Mungu kwa neema yako na kufanya naye agano jipya rejea kwa Mungu na
dhamiria kutembea katika njia zake kama walivyofanya manabii waliotutangulia,
endapo unaona yako maamuzi magumu ya kufanya tafadhali wasiliana na kiongozi
wako wa kiroho, na washauri wa maswala ya kiroho kuangalia athari za maamuzi
unayokwenda kuyafanya na muongozo wake
hasa kama kuna agano la kuweka sawa na kama una agano la malipizo, Kumbuka
agabo linapovunjwa linadai Damu, itumie Damu ya Yesu kwa msamaha wa kweli na
rehema na uwe na imani kuwa Damu hii inakunenea mema kuliko ile ya Habili.
Waebrania
12:24 “na Yesu mjumbe wa agano jipya, na damu ya
kunyunyizwa, inenayo mema kuliko ile ya Habili”
Hitimisho.
Agano wakati wote linahitaji kujitoa,
unapofanya agano na Mungu ni lazima uwe umemaanisha katika hilo unalolifanya,
watu wengi leo wanaingia katika maagano na kuyavunja kiwepesi kwa sababu
hawatambui gharama za agano hilo, ingawa Mungu ni wa rehema nafasi ya toba bado
ipo, na Mungu yuaweza kukurejeza kwake iwapo umeharibu, Mungu atawarehemu na
kuwapa neema wale wote wanaojinyenyekeza na kutafuta kumrudia yeye lakini ni
lazika ufanye au uchukue hatua madhubuti kujitoa katika nira zilizo kinyume na
mapenzi ya Mungu naye atakuwa baba yako nawe utakuwa mwanae wa kike na wa
kiume!
2Wakorintho
6:14-18 “Msifungiwe nira pamoja na wasioamini, kwa
jinsi isivyo sawasawa; kwa maana pana urafiki gani kati ya haki na uasi? Tena
pana shirika gani kati ya nuru na giza? Tena pana ulinganifu gani kati ya
Kristo na Beliari? Au yeye aaminiye ana sehemu gani pamoja na yeye asiyeamini?
Tena pana mapatano gani kati ya hekalu la Mungu na sanamu? Kwa maana sisi tu
hekalu la Mungu aliye hai; kama Mungu alivyosema, ya kwamba, Nitakaa ndani yao,
na kati yao nitatembea, nami nitakuwa Mungu wao, nao watakuwa watu wangu. Kwa
hiyo, Tokeni kati yao, Mkatengwe nao, asema Bwana, Msiguse kitu kilicho
kichafu, Nami nitawakaribisha. Nitakuwa Baba kwenu, Nanyi mtakuwa kwangu
wanangu wa kiume na wa kike,”
Na.
Rev. Innocent Samuel Kamote.
Mkuu
wa wajenzi mwenye Hekima!