Jumapili, 14 Septemba 2025

Urithi wa Mtoto wa kike!


Hesabu 27:1-4 “Wakati huo wakakaribia hao binti za Selofehadi, mwana wa Heferi, mwana wa Gileadi, mwana wa Makiri, mwana wa Manase, wa jamaa za Manase mwana wa Yusufu; na majina ya hao binti za Selofehadi ni haya; Mala, na Noa, na Hogla, na Milka, na Tirsa. Nao wakasimama mbele ya Musa, na mbele ya Eleazari kuhani, na mbele ya wakuu, na mkutano wote, mlangoni pa hema ya kukutania, wakasema, Babaetu alikufa nyikani, naye hakuwamo katika mkutano wa hao waliojikutanisha kinyume cha Bwana katika mkutano wa Kora; lakini akafa katika dhambi zake mwenyewe; naye alikuwa hana wana wa kiume. Kwa nini basi jina la babaetu kufutwa katika jamaa zake kwa sababu alikuwa hana mwana wa kiume? Tupe sisi urithi pamoja na ndugu zake babaetu.”



Utangulizi:

Ni muhimu kufahamu kuwa katika Jamii nyingi zamani na hata siku hizi, Mwanamke hakupewa nafasi kubwa katika urithi wa mali za baba yake hususani ardhi, Kulikuwa na sheria na mila nyingi zinazompa upendeleo mtoto wa kiume na kumpuuzia mtoto wa kike, Hapa Masaini Loiborosoit A, Wilayani Simanjirio, Mkoani Manyara niliko pia nimeikuta mila hii miongoni mwa jamii ya Kimaasai, Mila, Desturi na Sheria kama hii vilevile lilikuweko katika jamii ya Kiyahudi wakati wa Torati ya Musa, Lakini kupitia mabinti jasiri sana wana wa SELOFEHADI  yaani Mala, Noa, Hogla, Milka na Tirsa  wao waliwahi kutoa hoja mbele ya Musa na kuhani mkuu Eleazari na kisha hoja ikapelekwa kwa Mungu na Mungu akalazimika kubadilisha sheria na kutoa kibali kwamba watoto wa kike wana haki ya kurithi kama ilivyo kwa watoto wa kiume, ujasiri wao na uthubutu wao wa kuweza kumkabili Musa na hatimaye Mungu kubadili sheria kwaaji yao unaonyesha kuwa mabinti hawa walikuwa na ujasiri usiokuwa wa kawaida “uncommon boldness” katika tafiti zangu wakati wa maandalizi ya somo hili nilimuona mtu mmoja akiwaita mabinti hawa “Change Makers” yaani waleta mabadiliko, Hoja yao ilikuwa na mashiko jambo lililopelekea Mungu kubadili sheria kwaajili ya watoto wa kike

Hesabu 27:5-8 “Basi Musa akaleta neno lao mbele ya Bwana Bwana akanena na Musa, na kumwambia, Hao binti za Selofehadi wananena lililo haki; kweli utawapa milki ya urithi pamoja na ndugu za baba yao; nawe utawapa urithi wa baba yao. Kisha utanena na wana wa Israeli, na kuwaambia, Mtu akifa, naye hana mwana wa kiume, ndipo utampa binti yake urithi wake.”

Leo basi tutachukua muda kujifunza kwa njia ya uchambuzi somo hili Urithi wa Mtoto wa kike kwa kuzingatia vipengele vitatu vifuatavyo:-

 

·         Sheria isiyozingatia haki

·         Kuvunjwa kwa sheria isiyozingatia haki

·         Urithi wa mtoto wa kike

                 

Sheria isiyozingatia haki

Sheria ya Musa pamoja na Mila nyingi na Desturi za zamani zilikuwa zimezoeleka ya kwamba urithi wa mali pamoja na ardhi ulikuwa unaelekezwa kwa watoto wa kiume pekee, mtoto wa kiume wa kwanza akipokea urithi mara dufu yaani mara mbili kuliko wengine na wengine kwa kadiri ya sehemu zao, watoto wa kike hawakuhesabiwa, na kuwa kama mtu angefariki dunia bila kuwa na mtoto wa kiume basi mali zake zingerithiwa na Ndugu zake wa karibu na mabinti wangeolewa tu na kuwa na jina la familia nyingine, kimsingi pia wangeachwa bila kurithi lolote

Kumbukumbu 21:15-17 “Akiwa mtu yuna wake wawili, mmoja ampenda, mmoja hampendi, nao wamemzalia watoto, ampendaye na asiyempenda wote wawili; na yule mzaliwa wa kwanza akiwa ni wa mke asiyependwa; ndipo itakapokuwa ya kwamba siku atakayowarithisha wanawe alivyo navyo, asimweke mwana wa ampendaye kuwa mzaliwa wa kwanza mbele ya mwana wa asiyempenda, naye ndiye mzaliwa wa kwanza huyu; lakini amkubali mzaliwa wa kwanza mwana wa yule asiyempenda, kwa kumpa mafungu mawili katika vyote alivyo navyo; kwa maana ndiye mwanzo wa nguvu zake; haki ya mzaliwa wa kwanza ni yake yeye.”

Kwa hiyo Mwanzoni Mila na Desturi na Sheria za Kiebrania hazikuwa zimemfikiria hata kidogo mtoto wa kike, Sheria hii ilikuwa ni Sheria isiyozingatia haki, ilisababisha huzuni kwa mabinti kwani mali hususani ardhi ya baba yao ingekwenda kwa ndugu zake na wao wangeachwa mikono mitupu, Binti za wana wa Selofehadi yaliwakuta haya, na bila shaka waliyafikiri kwa kina na kuona kuwa hakuna haki hapo na sheria hiyo ni kandamizi kwao wakadai haki hiyo

Hesabu 27:1-4 “Wakati huo wakakaribia hao binti za Selofehadi, mwana wa Heferi, mwana wa Gileadi, mwana wa Makiri, mwana wa Manase, wa jamaa za Manase mwana wa Yusufu; na majina ya hao binti za Selofehadi ni haya; Mala, na Noa, na Hogla, na Milka, na Tirsa. Nao wakasimama mbele ya Musa, na mbele ya Eleazari kuhani, na mbele ya wakuu, na mkutano wote, mlangoni pa hema ya kukutania, wakasema, Babaetu alikufa nyikani, naye hakuwamo katika mkutano wa hao waliojikutanisha kinyume cha Bwana katika mkutano wa Kora; lakini akafa katika dhambi zake mwenyewe; naye alikuwa hana wana wa kiume. Kwa nini basi jina la babaetu kufutwa katika jamaa zake kwa sababu alikuwa hana mwana wa kiume? Tupe sisi urithi pamoja na ndugu zake babaetu.”

Mabinti wa Selofehadi walihuzunika kuona kwakuwa baba yao hakuwa na mtoto wa kiume, basi ndugu zake baba yao wangerithi mali na ardhi yake na mabinti zake wakiepo wangeachwa bila kitu, lakini baada ya kuchukua hatua za kijasiri na kumkabili Musa na Musa akamuuliza Mungu huo ukawa mwisho wa sheria kandamizi dhidi ya wanawake.

Tunajifunza kutoka kwa Mala, na Noa, na Hogla, na Milka, na Tirsa kwamba tunaweza kubadili lolote lisilo la haki kwa ujasiri na lolote lililo kandamizi kwa njia ya maombi na Mungu akasikiliza, Sheria na Kanuni yoyote iliyokinyume na lile tunalolihitaji na linalosimama kama haki yetu mbele za Mungu inaweza kuingiliwa kati kwa Sheria ya Kanuni ya kuomba kwa Mungu, Mabinti hawa kwa imani na ujasiri walimkabili Musa na Musa aliomba kwa Mungu na Mungu akabadili sheria, tunaweza kuomba lolote kwa jina la Yesu kwenda kwa Baba yetu wa Mbinguni na kubadilisha Sheria na Kanuni, Mila na Desturi kandamizi na uhuru wetu ukapatikana katika jina la Yesu Kristo.

Kuvunjwa kwa sheria isiyozingatia haki

Habari ya mabinti hawa inatufundisha kuwa tunaweza kubadili sheria, endapo tu tutasimama katika haki, na tunajifunza ya kuwa maombi yana nguvu ya kubadili sheria mila na desturi ambazo hazitutendei haki katika ulimwengu wa roho na mwili, wakati habari hii ikizungumzia kubadilishwa kwa sheria iliyopelekea wasichana au wanawake katika familia kuwa na haki ya kisheria ya kurithi, lakini tunajifunza pia kuwa tunaweza kubadili sheria za mila na desturi za aina yoyote ile kwa njia ya maombi ikiwa sheria hiyo au mila hizo au kanuni hizo hazijazingatia haki

Esta 4:15-16 “Basi Esta akawatuma ili wamjibu Mordekai, Uende ukawakusanye Wayahudi wote waliopo hapa Shushani, mkafunge kwa ajili yangu; msile wala kunywa muda wa siku tatu, usiku wala mchana, nami na wajakazi wangu tutafunga vile vile; kisha nitaingia kwa mfalme, kinyume cha sheria; nami nikiangamia, na niangamie.”  

Daniel 6:10-26 “Hata Danieli, alipojua ya kuwa yale maandiko yamekwisha kutiwa sahihi, akaingia nyumbani mwake, (na madirisha katika chumba chake yalikuwa yamefunguliwa kukabili Yerusalemu ;) akapiga magoti mara tatu kila siku, akasali, akashukuru mbele za Mungu wake, kama alivyokuwa akifanya tokea hapo. Basi watu hao wakakusanyika pamoja, wakamwona Danieli akiomba dua, na kusihi mbele za Mungu wake. Ndipo wakakaribia, wakasema mbele ya mfalme katika habari ya ile marufuku ya mfalme; Je! Hukuitia sahihi ile marufuku, ya kwamba kila mtu atakayeomba dua kwa Mungu awaye yote, au kwa mtu awaye yote, katika muda wa siku thelathini, ila kwako, Ee mfalme, atatupwa katika tundu la simba? Mfalme akajibu, akasema, Neno hili ni kweli, kama ilivyo sheria ya Wamedi na Waajemi isiyoweza kubadilika. Basi wakajibu, wakasema mbele ya mfalme, Yule Danieli, aliye mmoja wa wana wa wale waliohamishwa wa Yuda, hakujali wewe, Ee mfalme, wala ile marufuku uliyoitia sahihi, bali aomba dua mara tatu kila siku. Basi mfalme aliposikia maneno haya alikasirika sana, akakaza moyo wake ili kumponya Danieli; akajitaabisha kumwokoa hata jua likachwa. Ndipo watu wale wakakusanyika pamoja mbele ya mfalme, wakamwambia mfalme, Ee mfalme, ujue ya kuwa ni sheria ya Wamedi na Waajemi, lisibadilike neno lo lote lililo marufuku, wala amri yo yote iliyowekwa na mfalme. Basi mfalme akatoa amri, nao wakamleta Danieli, wakamtupa katika tundu la simba. Mfalme akanena, akamwambia Danieli, Mungu wako unayemtumikia daima, yeye atakuponya. Likaletwa jiwe, likawekwa mdomoni mwa lile tundu; naye mfalme akalitia muhuri kwa muhuri yake mwenyewe, na kwa muhuri ya wakuu wake, lisibadilike neno lo lote katika habari za Danieli. Kisha mfalme akaenda nyumbani kwake, akakesha usiku kucha, akafunga; na vinanda havikuletwa mbele yake; na usingizi wake ukampaa. Asubuhi mfalme akaondoka mapema, akaenda kwa haraka mpaka penye lile tundu la simba.Naye alipolikaribia lile tundu, akamlilia Danieli kwa sauti ya huzuni; mfalme akanena; akamwambia Danieli, Ee Danieli, mtumishi wa Mungu aliye hai, je! Mungu wako, unayemtumikia daima, aweza kukuponya na simba hawa? Ndipo Danieli akamwambia mfalme, Ee mfalme, uishi milele. Mungu wangu amemtuma malaika wake, naye ameyafumba makanwa ya simba, nao hawakunidhuru; kwa kuwa mbele zake mimi nalionekana kuwa sina hatia; tena, mbele yako, Ee mfalme, sikukosa neno. Basi mfalme akafurahi sana, akaamuru wamtoe Danieli katika lile tundu. Ndipo Danieli akatolewa katika lile tundu, wala dhara lo lote halikuonekana mwilini mwake, kwa sababu alikuwa anamtumaini Mungu wake. Mfalme akaamuru, nao wakawaleta wale watu waliomshitaki Danieli, wakawatupa katika tundu la simba, wao, na watoto wao, na wake zao; na wale simba wakawashinda wakaivunja mifupa yao vipande vipande, kabla hawajafika chini ya tundu. Ndipo mfalme Dario akawaandikia watu wa kabila zote, na taifa zote, na lugha zote, waliokaa juu ya uso wa dunia; Amani na iongezeke kwenu. Mimi naweka amri, ya kwamba katika mamlaka yote ya ufalme wangu watu watetemeke na kuogopa mbele za Mungu wa Danieli; maana yeye ndiye Mungu aliye hai, adumuye milele, na ufalme wake ni ufalme usioharibika, na mamlaka yake itadumu hata mwisho.”              

Tunaona katika mifano kadhaa hapo juu ya kuwa maombi yana uwezo wa kuingilia kati sheria za kawaida na mila za kawaida na hata za Mungu na kubadilisha mambo, mabinti hawa wenye ujasiri waliomkabili Musa kwa maombo yao na ufuatiliaji waliweza kusababisha mabadiliko ya sheria, walimrudisha Musa kwa Mungu na Mungu akafanya mabadiliko ya sheria kwaajili yao na wengine hata leo, kwa tukio lao Mungu alibadili kanuni na kuamua kuwapa haki

Luka 18:1-7 “Akawaambia mfano, ya kwamba imewapasa kumwomba Mungu sikuzote, wala wasikate tamaa. Akasema, Palikuwa na kadhi katika mji fulani, hamchi Mungu, wala hajali watu. Na katika mji huo palikuwa na mwanamke mjane, aliyekuwa akimwendea-endea, akisema, Nipatie haki na adui wangu. Naye kwa muda alikataa; halafu akasema moyoni mwake, Ijapokuwa simchi Mungu wala sijali watu,lakini, kwa kuwa mjane huyu ananiudhi, nitampatia haki yake, asije akanichosha kwa kunijia daima.Bwana akasema, Sikilizeni asemavyo yule kadhi dhalimu. Na Mungu, je! Hatawapatia haki wateule wake wanaomlilia mchana na usiku, naye ni mvumilivu kwao?

Mungu atampa haki yake kila mtu anayemkomalia katika maombi, Mungu aliwapa haki mabinti wa Selofehadi ya Kuwa kama mtu akifa bila mwana wa kiume basi urithi wake utapewa binti zake, asipokuwa na binti au mwana wa kiume basi watepea ndugu zake walio karibu na sheria hii ikawa agizo la kudumu kwa Israel hata leo, haya yakawa mapinduzi makubwa na ya kipekee kwa sababu kupitia wao na kwa mara ya kwanza katika mila na desturi za Kiyahudi wanawake walihesabika kuwa warithi halali wa mali na ardhi ya baba zao. Sio hivyo tu Mungu aliongezea baadaye kwamba ili mali hizo zisitawanyike kutoka kwenye kabila lao basi mabinti hao waolewe ndani ya koo zao ili urithi usihame kutoka kabila moja hadi lingine na hii haikuwanyima haki ya kurithi bali ilihifadhi urithi ule ndani ya ukoo na ndani ya kabila husika bila kutawanyika kwa jina na mali za Muhusika

Hesabu 36:1-10 “Kisha wale wakuu wa nyumba za mababa ya jamaa ya wana wa Gileadi, mwana wa Makiri, mwana wa Manase, katika jamaa za wana wa Yusufu, wakakaribia, na kunena mbele ya Musa, na mbele ya wakuu walio juu ya nyumba za mababa ya wana wa Israeli; wakasema, Bwana alimwagiza bwana wangu awape wana wa Israeli nchi kwa kupiga kura iwe urithi wao; tena bwana wangu aliagizwa na Bwana awape binti za Selofehadi ndugu yetu huo urithi wa baba yao. Wakiolewa na watu wa wana wa hizo kabila nyingine za wana wa Israeli, ndipo urithi wao utatwaliwa na kuondolewa katika urithi wa baba zetu, na hiyo kabila watakayotiwa ndani yake itaongezewa urithi wao; basi urithi huo utaondolewa katika kura ya urithi wetu. Tena itakapokuwapo hiyo yubile ya wana wa Israeli, ndipo urithi wa hiyo kabila ambayo wamekuwa ndani yake utaongezewa huo urithi wao; hivyo urithi wao utaondolewa katika urithi wa kabila ya baba zetu. Basi Musa akawaagiza wana wa Israeli kama neno la Bwana lilivyokuwa, akasema, Kabila ya wana wa Yusufu imenena yaliyo haki. Bwana ameagiza neno hili katika habari ya binti za Selofehadi, akasema, Na waolewe na waume wawapendao; lakini na waolewe katika jamaa ya kabila ya baba zao. Hivyo hapana urithi wo wote wa wana wa Israeli utakaotoka kabila hii kwenda kabila hii; kwa kuwa wana wa Israeli watashikamana kila mtu na urithi wa kabila ya baba zake. Na kila binti atakayemiliki urithi katika kabila yo yote katika wana wa Israeli, ataolewa katika jamaa moja ya kabila ya baba yake, ili wana wa Israeli wapate kumiliki kila mtu urithi wa baba zake. Hivyo hapatakuwa na urithi uwao wote utakaotoka kabila hii kwenda kabila hii; kwa kuwa kabila za wana wa Israeli zitashikamana kila mmoja na urithi wake mwenyewe. Basi hao binti za Selofehadi wakafanya kama Bwana alivyomwagiza Musa;”

Urithi wa mtoto wa kike

Moja ya fundisho lingine la msingi na la Muhimu tunalojifunza kutoka kwa mabinti wa Selofehadi ni kuwa tunajifunza namna Mungu anavyotaka sheria ya urithi wa mtoto wa kike kuzingatiwa, Ni kama neno la Mungu olinatoa wito kwa jamii kutokuwapuuzia watoto wa kike katika maswala mbalimbali ya kijamii, Kamwe jamii haipaswi kufikiri kuwa Mwanamke ni kiumbe wa daraja la chini, Haki zao zimendikwa katika Torati na zimethibitishwa na Mungu mwenyewe. Jamii inapaswa kuondoa dhana potofu ya kufikiri kuwa mwanamke hastahili urithi na kupingana na hilo ni kupingana na mpango wa Mungu, watoto wa kike wapewe kila wanachistahili katika familia zao, ikiwa ni pamoja na kuwaelimisha, kupinga ukatili na ubaguzi wa kijinsia, kutokuwatahiri wanawake na yote yanayowanyima haki kutokana na maumbile yao na kuwa jamii inapaswa kuacha mila na desturi za kizamani ambazo ni kandamizi.

Katika nyakati za agano jipya Mwanamke ana haki na mwanaume, Mtumwa na muajiri, Myahudi na Myunani wote wana haki sawa za kiroho, Kwa hiyo anapomuamini Yesu wote wanaonekana kuwa wamoja katika Kristo

Wagalatia 3:27-29 “Maana ninyi nyote mliobatizwa katika Kristo mmemvaa Kristo. Hapana Myahudi wala Myunani. Hapana mtumwa wala huru. Hapana mtu mume wala mtu mke. Maana ninyi nyote mmekuwa mmoja katika Kristo Yesu. Na kama ninyi ni wa Kristo, basi, mmekuwa uzao wa Ibrahimu, na warithi sawasawa na ahadi.”

Habari ya mabinti wa Selofehadi ni fundisho la kipekee kwamba Mungu ni mtetezi wa haki ya wote walio dhaifu na wanyonge na wale wanaokandamizwa katika jamii, ni somo kwamba Mungu hakubaliani na mila na desturi zinazowanyima haki wengine kwa sababu fulani fulani, kila mwanadamu ana nafasi yake na heshima yake mbele za Mungu na kila mwanadamu anastahili kushiriki Baraka zote za Mungu, Urithi wa mwanamke ni agizo la Mungu na sio upendeleo, Lakini ili urithi ubaki katika kabila lao na jina la baba yao lisipotee waliolewa na binamu zao, kimsingi baadaye watoto hao mabinti walikabidhiwa urithi ulioahidiwa na Musa mtumishi wa Mungu katika nchi ya Mkanaani

Yoshua 17:3-4 “Lakini Selofehadi, mwana wa Heferi, mwana wa Gileadi, mwana wa Makiri, mwana wa Manase, hakuwa na wana waume ila binti; na majina ya hao binti zake walikuwa wakiitwa Mala, na Noa, na Hogla, na Milka, na Tirsa. Nao wakakaribia mbele ya Eleazari, kuhani, na mbele ya Yoshua, mwana wa Nuni, na mbele ya mashehe, wakasema, Bwana alimwamuru Musa kutupa sisi urithi kati ya ndugu zetu; basi kwa kuiandama hiyo amri ya Bwana akawapa urithi kati ya ndugu za baba yao.”

Desturi ya kuwanyima watoto wa kike urithi hususani wa Ardhi imeleta mafarakano katika jamii nyingi duniani, ni Sheria,  Mila na Desturi ambayo imeleta ubaguzi wa kijinsia, lakini hiki ambacho Mungu alikifanya baada ya mabinti wa Selofehadi kimeleta mtazamo mpya wa kijamii na usawa wa kijinsia, hivyo sio tu swala la ardhi lakini watoto wasomeshwe na wasiozwe katika hali ya utoto, lakini wajaliwe na kutunzwa na kuhudumiwa kama watoto wengine, Katika sheria za kislamu watoto wa kike hupewa urithi japo ni nusu ya kile wanapewa wanaume, Lakini wale wenye mila mbovu zinazo-mbagua mtoto wa kike wafahamu tu kuwa Mungu anawathamini nao vilevile kama anavyothamini watoto wa kiume hivyo ni wakati sasa kwa jamii kubadilika ni wakati wa mabunge kutunga sheria zenye kuzingatia uaswa wa kijinsia na kuondoa mila potofu na kandamizi katika jamii na kuachia zile zenye manufaa  

Rev. Innocent Samuel Kamote

Mkuu wa wajenzi mwenye Hekima 

Jumapili, 7 Septemba 2025

Chembe ya ngano isipoanguka!


Yoahana 12:23-25 “Naye Yesu akawajibu, akasema, Saa imefika atukuzwe Mwana wa Adamu. Amin, amin, nawaambia, Chembe ya ngano isipoanguka katika nchi, ikafa, hukaa hali iyo hiyo peke yake; bali ikifa, hutoa mazao mengi. Yeye aipendaye nafsi yake ataiangamiza; naye aichukiaye nafsi yake katika ulimwengu huu ataisalimisha hata uzima wa milele.”



Utangulizi:

Leo tunachukua muda kiasi kutafakari maneno ya Bwana wetu Yesu Kristo aliyoyasema karibu na mwishoni kabisa mwa huduma yake Duniani, Yesu alikuwa ametembelewa na kundi kubwa la jamii ya watu wasiokuwa wayahudi, yaani Wayunani ambao kimsingi nao walikuwa na kiu na hamu na shauku ya kupata huduma ya Bwana wetu Yesu Kristo, Yesu anaiona shauku yao kama hitaji kubwa sana la kiroho kwa jamii ya watu wote duniani kama watu wanaomuhitaji Mungu na Mwokozi katika maisha yao, Hata hivyo kuhudumia jamii ya watu wote duniani kwa vyovyote vile kungemlazimu kutimiza mapenzi ya Mungu ya kufa msalabani ili aweze kuwa fidia ya wengi kama yanenavyo maandiko:-

Yohana 3:16 “Kwa maana jinsi hii Mungu aliupenda ulimwengu, hata akamtoa Mwanawe pekee, ili kila mtu amwaminiye asipotee, bali awe na uzima wa milele.”

Luka 2:34-35 “Simeoni akawabariki, akamwambia Mariamu mama yake, Tazama, huyu amewekwa kwa kuanguka na kuinuka wengi walio katika Israeli, na kuwa ishara itakayonenewa. Nawe mwenyewe, upanga utaingia moyoni mwako, ili yafunuliwe mawazo ya mioyo mingi.”

Akifafanua juu ya mauti yake huku akiunganisha na mafundisho yahusuyo kujikana nafsi, Yesu anatumia mfano wa wakulima wa ngano ili kufafanua kanuni ya kiroho ya kuleta mafanikio na kuzaa matunda mengi inavyogharimu maisha ya waanzilishi ili kuleta uzima kwa wengi au kwa ulimwengu na ndipo anapotumia mfano wa Chembe ya ngano (Yaani mbegu ya ngano) kwamba ili iweze kutoa mazao mengi ni lazima ife na kuzikwa na inapoota yaani kufufuka inasababisha mazao mengi sana.

Tutajifunza ujumbe huu Chembe ya ngano isipoanguka kwa kuzingatia vipengele vitatu vifuatavyo;-


·         Maana ya kuanguka kwa chembe ya ngano.

·         Chembe ya ngano isipoanguka!.

·         Faida za kuanguka kwa chembe ya ngano.


Maana ya kuanguka kwa chembe ya ngano.

Ni muhimu kufahamu kuwa Pamoja na ukulima wa zabibu, ufugaji wa wanyama wa aina mbalimbali,kama kondoo, mbuzi na ng’ombe, watu wa mashariki ya kati hususani Israel na baadhi ya waarabu ni watumiaji wazuri sana wa ngano kwaajili ya chakula na hasa mikate, sasa ili Yesu aweze kueleweka vizuri katika jamii yake alitumia mifano ya vitu vya karibu na vilivyozoeleka katika jamii yake ili aweze kuwasilisha ujumbe wa kiroho wenye maana inayoeleweka kwa watu wake, Yesu hapa anatumia mfano wa chembe ya ngano (yaani mbegu ya ngano) ambayo ili iweze kuzaa matunda mengi zaidi hutupwa au kuzikwa shambani na kisha inakufa katika udongo au ardhini na inapofufuka/kuota kama mmea na kuzaa inazalisha matunda au mbegu nyingine bora zaidi hii ndio kanuni ya kilimo.

Yohana 12:24 “Amin, amin, nawaambia, Chembe ya ngano isipoanguka katika nchi, ikafa, hukaa hali iyo hiyo peke yake; bali ikifa, hutoa mazao mengi.”

·         Chembe ya ngano kwa kiyunani (Greek) inaitwa “ho kokkos tou sitou” kwa kiingereza “a grainof wheat”  ikimaanisha mbegu ya ngano

·         Kuanguka  kwa kiyunani (Greek) linatumika neno Piptō linalomaanisha kuanguka chini kwa hiyari, au kuangushwa kwa kusudi au kupanda

·         Kufa  kwa kiyunani (Greek) linatumika neno apothnēskō linalomaanisha kufa kimwili au kufa kwa hiyari yaani kwa kiingereza “Self- denial” “Self-sacrificial” kujitoa dhabihu, kujikana au kujikataa au kujitoa sadaka.

Waebrania katika mtazamo wao kuhusu mbegu siku zote waliamini ndani ya mbegu kua kuna UZIMA, URITHI, na KIZAZI, walikuwa wanatambua kuwa uhai hauwezi kuendelea bila ya kuwako kwa mbegu, lakini ili mbegu iweze kuendeleza uhai na uzima na urithi na kizazi ni lazima mbegu hiyo itolewe kutoka kwenye kuhifadhiwa na itupwe katika moyo wa ardhi, kisha ife na izikwe na kuchipuka ndipo iweze kuendeleza kizazi kwa hiyo mbegu katika mukthadha wa wayahudi inaitwa ZERA ikimaanisha UZAO 

Mwanzo 22:12-18 “Malaika wa BWANA akamwita Ibrahimu mara ya pili kutoka mbinguni akasema, Nimeapa kwa nafsi yangu asema BWANA, kwa kuwa umetenda neno hili, wala hukunizuilia mwanao, mwanao wa pekee, katika kubariki nitakubariki, na katika kuzidisha nitauzidisha uzao wako kama nyota za mbinguni, na kama mchanga ulioko pwani; na uzao wako utamiliki mlango wa adui zao; na katika uzao wako mataifa yote ya dunia watajibarikia; kwa sababu umetii sauti yangu.”

Yesu alikuwa anatambua kwamba ni lazima ajidhabihu yeye mwenyewe kwaajili ya kuufikia ulimwengu, alifahamu wazi kuwa yeye hakuja kwaajili ya wayahudi pekee, bali alikuja kwaajili ya ulimwengu mzima, alifahamu kuwa anahitajika sio na wayunani pekee bali na ulimwengu mzima na kwa sababu hiyo, kujidhabihu kwaajili ya ulimwengu mzima kungerahisisha ukombozi utakaozaa matunda kwa Mungu wetu yaliyo mengi, Lakini wakati huo huo Yesu aliwataka wanafunzi wake wote ikiwa ni pamoja na wewe na mimi kuwa na ufahamu ya kuwa maisha ya uanzilishi wa kitu chchote yanahusisha kujitoa na kujidhabihu na matunda yake yangelikuja kuonekana mbeleni!, Yeye kama Uzao wa Ibrahimu ilikuwa ni lazima ajitoe sadaka yeye mwenyewe kwa hiyari ili mataifa yote waweze kubarikiwa

Tito 2:11-14 “Maana neema ya Mungu iwaokoayo wanadamu wote imefunuliwa; nayo yatufundisha kukataa ubaya na tamaa za kidunia; tupate kuishi kwa kiasi, na haki, na utauwa, katika ulimwengu huu wa sasa; tukilitazamia tumaini lenye baraka na mafunuo ya utukufu wa Kristo Yesu, Mungu mkuu na Mwokozi wetu; ambaye alijitoa nafsi yake kwa ajili yetu, ili atukomboe na maasi yote, na kujisafishia watu wawe milki yake mwenyewe, wale walio na juhudi katika matendo mema.”

Waefeso 5:1-2 “Hivyo mfuateni Mungu, kama watoto wanaopendwa; mkaenende katika upendo, kama Kristo naye alivyowapenda ninyi tena akajitoa kwa ajili yetu, sadaka na dhabihu kwa Mungu, kuwa harufu ya manukato.”

Maandiko hayo yanadhihirisha wazi kuwa kusulubiwa kwa Yesu Kristo halikuwa tukio la kupangwa na wazee na wakuu wa makuhani, lakini lilikuwa ni tukio la Yesu Kristo mwenyewe kujidhabihu na kukubali kufa na kufufuka kutoka kwa wafu ili atukomboe wanadamu, Yeye alikuwa  ni chembe ya ngano ambayo ilikuwa lazima ianguke ili kusababisha mazao mengi sana duniani.                      

Chembe ya ngano isipoanguka!.

Yoahana 12:23-25 “Naye Yesu akawajibu, akasema, Saa imefika atukuzwe Mwana wa Adamu. Amin, amin, nawaambia, Chembe ya ngano isipoanguka katika nchi, ikafa, hukaa hali iyo hiyo peke yake; bali ikifa, hutoa mazao mengi. Yeye aipendaye nafsi yake ataiangamiza; naye aichukiaye nafsi yake katika ulimwengu huu ataisalimisha hata uzima wa milele.”

Yesu anatumia msemo huu  wa chembe yaani mbegu ya ngano kama mfano (Metaphor)  kuonyesha kuwa mbegu ili iweze kuleta mavuno mengi sana ni lazima ianguke, izikwe ardhini kisha inapochipuka yaani kuota na kustawi inaleta mavuno makubwa sana, kanuni hii ni kanuni ya kilimo lakini ni kanuni ya kiroho na kanuni ya kawaida katika maisha.

Yesu anaonyesha kuwa wakati mwingine ili mtu aweze kuzaa matunda, hakuna budi watu wajikane nafsi na kujidhabihu kama yeye, lakini sio hivyo tu kuishi maisha ya kumfuata Yesu na kumpendeza vile vile kunahitaji kujikana nafsi, Ni lazima ujikane ili uweze kuishi maisha matakatifu nay a mfano, bila kujikana ni ngumu kuona mazao

Luka 9:22-25 “akisema, Imempasa Mwana wa Adamu kupata mateso mengi, na kukataliwa na wazee na wakuu wa makuhani na waandishi, na kuuawa na siku ya tatu kufufuka. Akawaambia wote, Mtu ye yote akitaka kunifuata, na ajikane mwenyewe, ajitwike msalaba wake kila siku, anifuate. Kwa kuwa mtu atakaye kuiponya nafsi yake ataiangamiza, na mtu atakayeiangamiza nafsi yake kwa ajili yangu ndiye atakayeisalimisha. Kwa kuwa yamfaa nini mtu kuupata ulimwengu wote, kama akijiangamiza, au kujipoteza mwenyewe?

Chembe ya ngano isipoanguka hakuna lolote linaloweza kutokea, watu wasipojidhabihu na kujioa hakuwezi kutokea mabadiliko yoyote chanya katika jamii, mambo mengi tunayoyaona duniani na kuyafurahia wakati mwingine yamegharimu maisha ya watu wengine lakini wengi wanafaidika leo kutokana na kuumia kwa watu wengine, hususani waanzilishi wa mambo, Imani, mataifa, ustawi, uanzishwaji wa taasisi yoyote ile, upatikanaji wa Amani na kadhalika, huwa haviwezi kupata usitawi bila watu kujikana, kujiyoa na kujidhabihu, maisha ya kujitoa kwaajili ya jamii yanaweza kuumiza wachache lakini yakanufaisha wengi, Leo hii tunaushangilia wokovu na kujivunia lakini yaligharimu maisha ya Mwana wa Mungu, Yesu Kristo aligharimika pale msalabani na kwa kupigwa kwake tumepona

Marie Curie ambaye ni mgunduzi wa tiba ya kutumia mionzi (Radiation in Medicine) alifariki dunia tarehe 04 Julai 1934 huko ufaransa akiwa na miaka 66, Mwanamke huyu aliyekuwa mwanasayansi alihatarisha maisha yake hata kufa baada ya kuathiriwa na mionzi hiyo alipokuwa anafanya kazi za kitafiti na matumizi ya tiba ya mionzi ya (radium and Plonium) ambayo leo imekuwa msaada mkubwa sana katika tiba ya kiuchunguzi ya mionzi kama X-Rays

Katika maisha wakati mwingine mambo hayawezi kutokea mpaka watu wengine wamesimama kidete na kuhatarisha maisha yao au hata kufa kwaajili ya kusababisha mabadiliko yatokee, Mahatma Gandhi alijitoa maisha yake kusababisha nchi ya India kupata uhuru wake  kutoka kwa waingereza akianzisha harakati za kuandamana bila kufanya ghasia, akivumilia vifungo mbalimbali na hata wakati mwingine aliacha kula yaani akifunga na kujinyima ili haki za kibinadamu zipatikane  katika India inayofurahia matunda ya uhuru huo leo.

Wakristo, na watumishi wa Mungu katika mazingira mbalimbali, tunapaswa kuelewa Yesu alikuwa anamaanisha kwamba bila wengine kujitoa muhanga, maisha yao, fedha zao, starehe zao, mifungo yao, kesha zao, maisha ya familia zao, haki, na injili haiwezi kuwafikia watu wa Mungu, umasikini hauwezi kuondoka, unyonge hauwezi kuisha, ukandamizwaji hauwezi kukomeshwa, udhalimu hauwezi kutokomea, maovu yataendelea kuongezeka, amani haiwezi kupatikana, ubaguzi hauwezi kuisha, upendeleo hauwezi kuisha, haki haiwezi kupatikana, na uhuru wa kweli hauwezi kupatikana bila baadhi ya watu kujitoa dhabihu yaani  Chembe ya ngano isipoanguka! Inabakia ile ile!

Faida za kuanguka kwa chembe ya ngano.

Kuanguka kwa chembe ya ngano ni kujitoa au kujidhabihu kwaajili ya Mungu, Neno la Mungu linatueleza kuwa kujitoa ndio dhabihu iliyo hai, takatifu na ya kupendeza, kama mtu anataka kumpendeza Mungu basi ni lazima akubali kujitoa, au kujidhabihu, Kwa nini Mungu alipendezwa na Yesu Kristo hata kujivunia kuwa huyu ndiye mwanangu mpendwa ninayependezwa naye? Sababu kubwa ni kuwa Yesu alijitoa yeye mwenyewe

Warumi 12:1 “Basi, ndugu zangu, nawasihi, kwa huruma zake Mungu, itoeni miili yenu iwe dhabihu iliyo hai, takatifu, ya kumpendeza Mungu, ndiyo ibada yenu yenye maana.”

Wafilipi 2:6-11 “ambaye yeye mwanzo alikuwa yuna namna ya Mungu, naye hakuona kule kuwa sawa na Mungu kuwa ni kitu cha kushikamana nacho; bali alijifanya kuwa hana utukufu, akatwaa namna ya mtumwa, akawa ana mfano wa wanadamu; tena, alipoonekana ana umbo kama mwanadamu, alijinyenyekeza akawa mtii hata mauti, naam, mauti ya msalaba. Kwa hiyo tena Mungu alimwadhimisha mno, akamkirimia Jina lile lipitalo kila jina; ili kwa jina la Yesu kila goti lipigwe, la vitu vya mbinguni, na vya duniani, na vya chini ya nchi; na kila ulimi ukiri ya kuwa YESU KRISTO NI BWANA, kwa utukufu wa Mungu Baba.”

Mwanafunzi wa kweli wa Yesu Kristo ni yule anayejitoa, unapodai kuwa unamfuata Yesu lakini hujitoi maana yake ni sawa na kuwa hauufuati mfano wake, Yeye mwenyewe anamkana kila mtu anayedai kuwa anamfuata yeye lakini hataki kuteseka kwaajili ya Kristo! Kimsingi huwezi kuwa mwanafunzi wa Yesu kama hutaki kugharimika na kumfuata

Luka 14:27 “Mtu ye yote asiyeuchukua msalaba wake na kuja nyuma yangu, hawezi kuwa mwanafunzi wangu.”

Kila anayejikana kwaajili ya Yesu Kristo na jamii nafsi yake haitapotea kwani atalipwa uzima wa milele, tunapojitoa na kujidhabihu hata kufa kwaajili ya wengine/kifo au mauti yako inayotokana na kujidhabihu haiwi mwisho badala yake unakuwa mwanzo wa uzima na maisha mapya yenye Baraka nyingi na yenye kukuzalia matunda

Isaya 53:5-11 “Bali alijeruhiwa kwa makosa yetu, Alichubuliwa kwa maovu yetu; Adhabu ya amani yetu ilikuwa juu yake, Na kwa kupigwa kwake sisi tumepona. Sisi sote kama kondoo tumepotea; Kila mmoja wetu amegeukia njia yake mwenyewe; Na Bwana ameweka juu yake Maovu yetu sisi sote. Alionewa, lakini alinyenyekea, Wala hakufunua kinywa chake; Kama mwana-kondoo apelekwaye machinjoni, Na kama vile kondoo anyamazavyo Mbele yao wakatao manyoya yake; Naam, hakufunua kinywa chake. Kwa kuonewa na kuhukumiwa aliondolewa; Na maisha yake ni nani atakayeisimulia? Maana amekatiliwa mbali na nchi ya walio hai; Alipigwa kwa sababu ya makosa ya watu wangu. Wakamfanyia kaburi pamoja na wabaya; Na pamoja na matajiri katika kufa kwake; Ingawa hakutenda jeuri, Wala hapakuwa na hila kinywani mwake. Lakini Bwana aliridhika kumchubua; Amemhuzunisha; Utakapofanya nafsi yake kuwa dhabihu kwa dhambi, Ataona uzao wake, ataishi siku nyingi, Na mapenzi ya Bwana yatafanikiwa mkononi mwake; Ataona mazao ya taabu ya nafsi yake, na kuridhika. Kwa maarifa yake mtumishi wangu mwenye haki Atawafanya wengi kuwa wenye haki; Naye atayachukua maovu yao.”     

Yoahana 12:25-26 “Yeye aipendaye nafsi yake ataiangamiza; naye aichukiaye nafsi yake katika ulimwengu huu ataisalimisha hata uzima wa milele. Mtu akinitumikia, na anifuate; nami nilipo, ndipo na mtumishi wangu atakapokuwapo. Tena mtu akinitumikia, Baba atamheshimu.”

Hitimisho.

Kuishi maisha matakatifu kunahitaji kujikana, kuishi kwaajili ya Kristo kunahitaji kujikana, kuwatumikia watu kunahitaji kujikana, kuanzisha kazi mpya kunahitaji kujikana, kufanya umisheni kunahitaji kujikana, kumtumikia Mungu kunahitaji kujikana, kufanya uinjilisti kunahitaji kujikana, kuimba kwaya kunahitaji kujikana, kuomba kunahitaji kujikana, kukesha kunahitaji kujikana, kila kitu duniani na mafanikio yoyote yale duniani hayawezi kuja kama hatuna kujikana, kuleta maendeleo kunahitaji kujikana, bila kujikana katika jambo lolote lile hakuwezi kuwako na matunda yanayokusudiwa, mwanafunzi ili afaulu mitihani yake anahitaji kujikana, kusoma kunahitaji kujikana, biashara inahitaji kujikana, kilimo kinahitaji kujikana maendeleo yoyote yake yanahitaji kujikana hali kadhalika maisha ya kiroho yanahitaji kujikana hii ndio kanuni ya mafanikio, ni lazima chembe ya ngano ianguke, isipoanguka inabakia ile ile, lakini ikifa ikizikwa inatoa mazao mengi sana hii ni kanuni ya wokovu, ni kanuni ya kiroho na ni kanuni ya maisha,  na ni kanuni ya kuleta mafanikio makubwa duniani chembe ya ngano isipoanguka ikafa, hukaa hali iyo hiyo peke yake; bali ikifa, hutoa mazao mengi, Ni dua yangu na maombi yangu wasomaji wangu na wasilikizaji wangu tujitoe kwaajili ya kazi ya Mungu kabla ya kuangalia faida zetu binafsi.               

1Wakorintho 15:36-38 “Ewe mpumbavu! Uipandayo haihuiki, isipokufa; nayo uipandayo, huupandi mwili ule utakaokuwa, ila chembe tupu, ikiwa ni ya ngano au nyingineyo; lakini Mungu huipa mwili kama apendavyo, na kila mbegu mwili wake.”

Na. Rev. Innocent Samuel Kamote.

Mkuu wa wajenzi mwenye hekima.

+255718990796

Jumapili, 31 Agosti 2025

Tazama nimekupa mlango uliofunguliwa!


Ufunuo 3:7-8 “Na kwa malaika wa kanisa lililoko Filadelfia andika; Haya ndiyo anenayo yeye aliye mtakatifu, aliye wa kweli, aliye na ufunguo wa Daudi, yeye mwenye kufungua wala hapana afungaye, naye afunga wala hapana afunguaye. Nayajua matendo yako. Tazama, nimekupa mlango uliofunguliwa mbele yako, ambao hapana awezaye kuufunga, kwa kuwa unazo nguvu kidogo, nawe umelitunza neno langu, wala hukulikana jina langu.”



Utangulizi:

Ni muhimu kufahamu kuwa katika maisha yetu kama wanadamu ziko nyakati ambazo tunaweza kujikuta katika dimbwi la mawazo na hali ya kutokufahamu kutokana na mambo kadhaa katika maisha yetu kutokuenenda kama tunavyotaka au kufikiri,  na mara nyingine tumejikuta hatuelewi au kuwa kama watu waendao gizani kwa kupapasa kwa sababu tu ya kutokuyajua mapenzi ya Mungu katika maisha yetu, tunaweza kudhani kuwa labda tuko katika maisha yaliyopoteza mwelekeo, au yaliyopoteza tumaini, na kukosa msaada ya kiungu au hata wa kibinadamu wakati mwingine unaweza kuwaza hata kufikiri kuwa labda una laana, au kuna mtu amekuroga kwa sababu tu huoni mwelekeo wa hatima ile unayoitamani katika maisha yako huu ni ule wakati ambapo tumekwama na kila mlango wa mpenyo tuliojaribu katika maisha yetu unaonekana kama umefungwa au umepata kile ambacho hakilingani na akili yako au mtazamo wako au kile ulichokitarajia! Mlango umefungwa! Unaweza kufikiria kuwa umekataliwa kila mahali na ukadhania kuwa hustahili na ni kama Mungu hausiki na maisha yako tena lakini Mungu anajua uliposimama na ameahidi kufanya kitu kwako!

Isaya 22:19-22 “Nami nitakusukuma na kukutoa katika mahali pako, naye atakushusha utoke hapa usimamapo. Na itakuwa katika siku ile nitamwita mtumishi wangu Eliakimu, mwana wa Hilkia; nami nitamvika vazi lako, nitamtia nguvu kwa mshipi wako, nami nitamkabidhi yeye mamlaka yako; naye atakuwa baba kwa wenyeji wa Yerusalemu, na kwa nyumba ya Yuda. Na ufunguo wa nyumba ya Daudi nitauweka begani mwake; yeye atafungua wala hapana atakayefunga; naye atafunga wala hapana atakayefungua.”

Leo tutachukua muda kutafakari mambo haya yanayotokeza katika maisha yetu kwa kuliangalia neno la Mungu linasema nini pale tunapohisi kuwa labda mlango huu umefunga, labda jaribu hili halitatoka, na pale unapohisi umekwama, leo tutajikumbusha kuwa neno la Mungu linaonyesha wazi kuwa hakuna mwanadamu anaweza kukufunga wala mchawi anayeweza kuzuia Baraka zako kwa sababu tunaye Mungu mwenye mamlaka ya kufunga na kufungua milango na hakuna mtu anayeweza kufunga alichokifungulia wala hakuna anayeweza kufungua alichokifunga, Yeye ndiye anayesema leo Tazama nimekupa mlango uliofunguliwa! Na tutajifunza somo hili kwa kuzingatia vipengele vitatu vifuatavyo:-


·         Maana ya mlango uliofunguliwa.

·         Tazama nimekupa mlango uliofunguliwa.

·         Na huyu ndiye mwenye mamlaka ya milango yote.   

      

Maana ya mlango uliofunguliwa.

Kwa kawaida neno mlango uliofunguliwa  katika maandiko una maana pana sana neno uliofunguliwa katika lugha ya kiebrania linatumika neno “Pāthah”  na neno lingine la kiebrania ni “Gālāh” kwa kiyunani “AnoigōKwa hiyo neno Mlango uliofunguliwa kwa kiyunani linasomeka “Anoigō thura” neno hili lilitumika kumaanisha kupata mpenyo, kufunguliwa macho, kufunguliwa kinywa, kufunguliwa masikio, kufunguliwa mlango, kupewa macho ya kuona, kufunguliwa mbingu, kuwekewa wazi, kupata nafasi, kutoka, na kupata muelekeo, kwa sababu hiyo Mlango katika lugha ya kiroho unawakilisha Nafasi maalumu anayoitoa Mungu kwa mwanadamu kwaajili ya huduma, kusonga mbele, kutoka katika changamoto inayokukabili katika maisha kwa msaada wa Mungu  na anayesababisha milango hiyo ifunguke ni Mungu mwenyewe na hufanya hivyo kwa watu wake ambao pia ni kondoo wa malisho yake! Yesu alikwisha kutangaza kuwa yeye ndio mlango wa kondoo, awaye yote ambaye anataka upenvyo wa aina yoyote katika maisha yake hawezi kutoka bila kupitia Yesu!

Yohana 10:7-10 “Basi Yesu aliwaambia tena, Amin, amin, nawaambieni, Mimi ndimi mlango wa kondoo. Wote walionitangulia ni wevi na wanyang'anyi; lakini kondoo hawakuwasikia. Mimi ndimi mlango; mtu akiingia kwa mimi, ataokoka; ataingia na kutoka, naye atapata malisho. Mwivi haji ila aibe na kuchinja na kuharibu; mimi nalikuja ili wawe na uzima, kisha wawe nao tele.”

Kwa msingi huu katika maisha yetu tunapoona kuwa kuna mambo hayaendi katika maisha yetu ya kila siku hatupaswi kuzimia moyo kwa sababu uko mlango uliofunguliwa kwaajili yetu na yuko mwenye mamlaka ya kufunga na kufungua, hakuna mtu awaye yote anayeweza kuzuia usiolewe, hakuna mtu anayeweza kuzuia usifanikiwe, hakuna mtu anayeweza kuzuia usizae, hakuna mtu anayeweza kuzuia usipate kazi, hakuna mtu anayeweza kuzuia usifanikiwe, hakuna mtu anayeweza kuzuia usipone,  hakuna mtu anayeweza kuzuia usijenge hakuna mtu anayeweza kuzuia usiendelee mbele, hakuna anayeweza kuzuia usifaulu! Mungu wetu sio binadamu, hakuna mnyanyasaji asiyekuwa na mwisho, hakuna adui asiyekuwa na mwisho, hakuna hali ngumu isiyokuwa na mwisho kwa sababu uko mlango uliofunguliwa kwaajili yako, Mungu amekupa mlango uliofunguliwa wengine wanaweza kuona giza lakini sivyo itakavyokuwa kwako wewe na mimi wewe na mimi neno la Mungu linatuambia kuwa tunao mlango ulio wazi nguvu ya mafanikio iko kwetu na Mungu anayeweza kutufanikisha yuko kwetu na yeye ndio mlango wenyewe!

Tazama nimekupa mlango uliofunguliwa

Ni muhimu kuelewa kuwa wakati tunapopitia changamoto na majaribu mbalimbali moja ya kazi kubwa anayoifanya Shetani au adui ni kutufanya tusione njia, yaani ni kutupofusha tusipate ufunuo wa mapenzi na makusudi ya Mungu na hii ndio inayotufanya tufadhaike na kuvunjika moyo au kukata tamaa kwa sababu ya hali unayoipita kwa wakati ule, lakini Neno la Mungu linasema kuwa kwa kila jaribu uko mlango wa kutokea, na Mungu amekupa mlango uliofunguliwa!

2Wakorintho 4:3-4 “Lakini ikiwa injili yetu imesitirika, imesitirika kwa hao wanaopotea; ambao ndani yao mungu wa dunia hii amepofusha fikira zao wasioamini, isiwazukie nuru ya injili ya utukufu wake Kristo aliye sura yake Mungu.”

1Wakorintho 10:13 “Jaribu halikuwapata ninyi, isipokuwa lililo kawaida ya wanadamu; ila Mungu ni mwaminifu; ambaye hatawaacha mjaribiwe kupita mwezavyo; lakini pamoja na lile jaribu atafanya na mlango wa kutokea, ili mweze kustahimili.”    

Ufunuo 3:7-8 “Na kwa malaika wa kanisa lililoko Filadelfia andika; Haya ndiyo anenayo yeye aliye mtakatifu, aliye wa kweli, aliye na ufunguo wa Daudi, yeye mwenye kufungua wala hapana afungaye, naye afunga wala hapana afunguaye. Nayajua matendo yako. Tazama, nimekupa mlango uliofunguliwa mbele yako, ambao hapana awezaye kuufunga, kwa kuwa unazo nguvu kidogo, nawe umelitunza neno langu, wala hukulikana jina langu.”

Mungu ametupa mlango uliofunguliwa, hakuna mtu wa Mungu ambaye anaweza kukwama milele, Mungu anapofunga mlango mmoja huwa anafungua mlango mwingine, kila mwanadamu anayejitahidi kukuzibia ataula wa chuya kwa uvivu wa kuchambua, hajui nguvu na uweza wa Mungu wetu sisi tunao ufunguo wa Daudi, kila mahali palipofungwa tutatoboa tu, ni lazima ufahamu ya kuwa wakati mwingine unapoona mambo yanakwama sio lazima iwe umerogwa wewe haurogeki sio lazima uwe una laana wewe haulaniki, lakini wakati mwingine ni sauti ya Mungu inafunga mlango mmoja ili kufungua mwingine, na ukisikiliza katika ulimwengu wa roho kwa makini mlango uko wazi kwako na kwaajili yako!

Matendo 16:6-10 “Wakapita katika nchi ya Frigia na Galatia, wakikatazwa na Roho Mtakatifu, wasilihubiri lile neno katika Asia. Walipofika kukabili Misia wakajaribu kuenda Bithinia, lakini Roho wa Yesu hakuwapa ruhusa, wakapita Misia wakatelemkia Troa. Paulo akatokewa na maono usiku; alimwona mtu wa Makedonia amesimama, akimsihi, na kumwambia, Vuka, uje Makedonia utusaidie. Basi alipokwisha kuyaona yale maono, mara tukataka kutoka kwenda Makedonia, kwa kuwa tuliona hakika ya kwamba Mungu ametuita tuwahubiri Habari Njema.”

-          Walimfanyia fitini Yusufu, walimtupa shimoni, walimuuza utumwani Misri, walimfitini tena na alitupwa gerezani, badala ya mema ilionekana kana kwamba mambo yanamuendea vibaya lakini katika mpango wa Mungu, Mungu alikuwa anatengeneza mlango uliofunguliwa wa kumuweka Yusufu katika ufalme

 

Mwanzo 41:40-44 “Basi wewe utakuwa juu ya nyumba yangu, na kwa neno lako watu wangu watatawaliwa. Katika kiti cha enzi tu nitakuwa mkuu kuliko wewe. Farao akamwambia Yusufu, Tazama, nimekuweka juu ya nchi yote ya Misri. Farao akavua pete yake ya muhuri mkononi mwake, akaitia mkononi mwa Yusufu; akamvika mavazi ya kitani nzuri, na kumtia mkufu wa dhahabu shingoni mwake. Akampandisha katika gari lake la pili alilokuwa nalo. Na watu wakapiga kelele mbele yake, Pigeni magoti. Hivyo akamweka juu ya nchi yote ya Misri. Farao akamwambia Yusufu, Mimi ni Farao, na bila amri yako, mtu asiinue mkono wala mguu katika nchi yote ya Misri.”

 

-          Walimdharau Daudi na kufikiri ya kuwa hafai kabisa kuwa miongoni mwa watoto anayeweza kuwa mfalme na kupakwa mafuta, alipigwa vita kila mahali, hakukubaliwa na baba wala hakukubaliwa na kaka zake, na mfalme aliyekuwepo madarakani alimkataa na kutaka kumuua, alimwinda katika mapango na kujaribu kwa kila jinsi na kila namna kumzuia asiwe mfalme, njia ilionekana kuwa ngumu milango ilionekana kufunga lakini Mungu alikuwa na sababu, hatimaye Yeye akawa ndiye mtu sahihi aliyeupendeza Moyo wa Mungu na aliyewaongoza Israel kwa ukamilifu wa moyo, Mungu alimpa Daudi mlango uliofunguliwa!

 

Zaburi 78:70-72 “Akamchagua Daudi, mtumishi wake, Akamwondoa katika mazizi ya kondoo. Nyuma ya kondoo wanyonyeshao alimwondoa, Awachunge Yakobo watu wake, na Israeli urithi wake. Akawalisha kwa ukamilifu wa moyo wake, Na kuwaongoza kwa busara ya mikono yake.”

 

-          Walimfukuza Hajiri na Ishamel na kuwatupilia jangwani, waliishiwa na mkate na waliishiwa na maji na hatari ya kifo ilikuwa ikiwakabili, Hajiri alilia na Ishamel alilia Lakini Mungu ni Mungu ambaye hakuwa na upendeleo aliwafungulia mlango wa uhai hata walipokuwa wametaka tamaa jangwani Mungu alijidhihirisha kuwa ni Mungu mwenye kujali ni Mungu mwenye upendo, ni Mungu asiye na upendeleo, Ni Mungu anayebariki na ni Mungu mwenye kukuza sana aliahidi kumfanya Ishamel kuwa Taifa kubwa hakuna upendeleo kwa Mungu!

 

Mwanzo 21:10-21 “Kwa hiyo akamwambia Ibrahimu, Mfukuze mjakazi huyu na mwanawe, maana mwana wa mjakazi hatarithi pamoja na mwanangu, Isaka. Na neno hilo lilikuwa baya sana machoni pa Ibrahimu, kwa ajili ya mwanawe. Mungu akamwambia Ibrahimu, Neno hili lisiwe baya machoni pako, kwa ajili ya huyo mwana, na huyo mjakazi wako. Kila akuambialo Sara, sikiza sauti yake, kwa maana katika Isaka uzao wako utaitwa. Naye mwana wa mjakazi nitamfanya kuwa taifa, maana huyu naye ni uzao wako. Ibrahimu akaamka asubuhi na mapema akatwaa mkate na kiriba cha maji, akampa Hajiri akimtwika begani pake, na kijana, akamruhusu; naye akatoka, akapotea katika jangwa la Beer-sheba. Yale maji yakaisha katika kiriba, akamlaza kijana chini ya kijiti kimoja. Akaenda akakaa akimkabili, mbali naye kadiri ya mtupo wa mshale; maana alisema, Nisimwone kijana akifa; naye akakaa akimkabili, akapaza sauti yake, akalia. Mungu akasikia sauti ya kijana. Malaika wa Mungu akamwita Hajiri kutoka mbinguni, akamwambia, Una nini, Hajiri? Usiogope, maana Mungu amesikia sauti ya kijana huko aliko. Ondoka, ukamwinue kijana, ukamshike mkononi mwako, kwa kuwa nitamfanya kuwa taifa kubwa. Mungu akamfumbua macho, naye akaona kisima cha maji; akaenda akakijaza kiriba maji, akamnywesha kijana. Mungu akawa pamoja na huyo kijana, naye akakua, akakaa katika jangwa, akawa mpiga upinde. Akakaa katika jangwa la Parani; mama yake akamtwalia mke katika nchi ya Misri.”

Ndugu yangu Mungu ametupa mlango uliofunguka, haijalishi sasa unapitia hali ya namna gani, au umesimama katika hali inayoonekana kuwa ni ngumu na kama kila kitu hakionekani kuwa sawasawa huna sababu ya kulalamika wala kunung’unika  Mungu anaweza kukufungulia mlango wa afya yako, masomo yako, visa yako, safari yako, biashara zako, cheo chako, mshahara wako kuongezeka, mapato yako kuchanua, kilimo na biashara kufanikiwa, walikuwa wakifukia visima vya Isaka lakini aliendelea kuchimba vingine hakuna mtu anaweza kukufungia mlango, njia za Mungu sio kama njia za wanadamu wala mawazo yake sio kama mawazo yetu yeye huweza kufanya njia pasipo na njia leo Mungu amenituma nikukumbushe ya kuwa uko mlango uliofunguliwa kwaajili yako, ndoa yako njema inakuhusu, mchumba anakuja na yule aliyeondoka haikuwa mpango wa Mungu Mungu atakufungulia mlango mwingine, kazi iliyopotea haikuwa mahali pako sahihi Mungu amekupa mlango ulio wazi Mungu amekupa mlango uliofunguliwa na hakuna awezaye kuufunga. 

Na huyu ndiye mwenye mamlaka ya milango yote

Ufunuo 3:7 “Na kwa malaika wa kanisa lililoko Filadelfia andika; Haya ndiyo anenayo yeye aliye mtakatifu, aliye wa kweli, aliye na ufunguo wa Daudi, yeye mwenye kufungua wala hapana afungaye, naye afunga wala hapana afunguaye.”

Yesu Kristo ndiye aliyejitangaza ya kuwa anao ufunguo na kuwa mwenye kufunga ni yeye na mwenye kufungua ni yeye na akifunga hapana afunguae na akifungua hakuna awezaye kufunga, huna sababu ya kulalamika wala kulia unapoona mambo hayaendi, Yesu anabatiza kwa Roho Mtakatifu, Yesu anamwaga neema juu ya neema, Yesu ndiye anayebariki, Yesu ndiye anayefungua kurasa mpya wakati nyingine inapofunga yeye anayo mamlaka yote, Yesu sio tu anafungua milango yote lakini pia anazo funguo za mauti na kuzimu hakuna wa kukupeleka kaburini bila ruhusa yake na uwezo wake, watu wanaweza kukuona umekwama lakini Yesu anakuona unaelekea anakotaka uko mlango na unaweza kuwekwa wazi kwako katika ndoa yako, katika maisha yako, katika magonjwa yako, katika familia yako, katika uponyaji wako, acha kuangalia milango iliyofungwa mwangalie mwenye funguo mwangalie Yesu ambaye yeye ana mamlaka na wokovu wako, na uponyaji wako na mafanikio yako ukimwangalia yeye kutoboa utatoboa katika jina la Yesu Kristo mwana wa Mungu aliye hai kataa kuona giza, kataa mahangaiko mwombe Bwana akufungulie mlango, Mwambie nipe kuona Malango uliofunguliwa nionapo giza naye amekupa mlango uliofunguliwa tayari!

Ufunuo 1:17-18 “Nami nilipomwona, nalianguka miguuni pake kama mtu aliyekufa. Akaweka mkono wake wa kuume juu yangu, akisema, Usiogope, Mimi ni wa kwanza na wa mwisho, na aliye hai; nami nalikuwa nimekufa, na tazama, ni hai hata milele na milele. Nami ninazo funguo za mauti, na za kuzimu.”     

 

Na Rev. Innocent Samuel Kamote

 

Mkuu wa wajenzi mwenye Hekima!

Jumapili, 24 Agosti 2025

Basi sasa unipe mlima huu!


Yoshua 14:12-13Basi sasa unipe mlima huu, ambao Bwana alinena habari zake siku hiyo; kwani wewe ulisikia siku hiyo jinsi Waanaki walivyokuwa huko, na miji ilivyokuwa mikubwa yenye boma; yumkini yeye Bwana atakuwa pamoja nami, nami nitawafukuza watoke nje, kama Bwana alivyonena. Yoshua akambarikia, akampa Kalebu, huyo mwana wa Yefune, Hebroni kuwa urithi wake.”



Utangulizi:

Leo tutakuwa na muda wa kutafakari sehemu mojawapo muhimu ya kitabu cha Yoshua katika kifungu cha Yoshua 14:6-13, ambapo kimsingi tunaweza kupata mafundisho ya kushangaza sana tunayoyapata kutoka kwa Kalebu mmoja wa wapelelezi 12 waliotumwa na Musa kuichunguza nchi ya Kanaani. Ni jambo la kushangaza kwamba Mungu hakuwa amemsahahu mtu huyu sawasawa na ahadi yake aliyompatia kwa kinywa cha Musa mtumishi wake, kimsingi wakati mwingi sana ulikuwa umepita na sasa Kalebu ana miaka 85 lakini bado anaonyesha imani thabiti kwa Mungu, uvumilivu na ukakamavu na kama mtu mwenye subira kubwa na tumaini la maisha asiyekata tamaa, ambapo licha ya muda mrefu kuwa umepita anaikumbushia ile ahadi, huku akiwa tayari kuipambania haki yake aliyoahidiwa na Mungu, baada ya watu wengine wote kuogopa kuingia katika nchi ya Mkanaani na kupambana na majitu yaliyokuwa yanaimiliki nchi hiyo na Mungu akamuahidi Kalebu na Yoshua.

Hesabu 14:28-31 “Waambieni, Kama niishivyo, asema Bwana, hakika yangu kama ninyi mlivyonena masikioni mwangu, ndivyo nitakavyowafanyia ninyi; mizoga yenu itaanguka katika jangwa hili, na wote waliohesabiwa miongoni mwenu, kama jumla ya hesabu yenu, tangu waliopata umri wa miaka ishirini na zaidi, hao walioninung'unikia, hakika yangu hamtaingia ninyi katika nchi, ambayo niliinua mkono wangu ya kwamba nitawaketisha humo, isipokuwa Kalebu mwana wa Yefune, na Yoshua mwana wa Nuni. Lakini Watoto wenu, ambao mlisema watakuwa mateka, ndio nitakaowaleta na kuwatia ndani, nao wataijua nchi ninyi mliyoikataa.”

Tutajifunza ujumbe huu muhimu “Basi sasa unipe mlima huu” kwa kuzingatia vipengele vitatu vifuatavyo:-

·         Sababu za ahadi ya Mungu kwa Kalebu na Yoshua.

·         Basi sasa unipe mlima huu.

·         Mambo ya kujifunza kutoka kwa Kalebu.


Sababu za ahadi ya Mungu kwa Kalebu na Yoshua.

Ni muhimu kufahamu kwanza ni kwanini Mungu aliwapenda na kuwaahidi Kalebu na Yoshua kwamba watairithi nchi ya Kanaani tofauti na wenzao miongoni mwa wapelelezi 12 waliotumwa na Musa kuipeleleza nchi ya Kanaani, ili tuweze kujifunza kutoka kwake na kuwa na moyo kama wa Kalebu na Yoshua hatimaye nasi tuweze kuzifurahia Baraka za Mungu. Kalebu na Yoshua walikuwa ni askari waaminifu na watiifu kwa Mungu, wote walikuwa wametokea Misri katika nchi ya utumwa wakiwa vijana wadogo, na walipata bahati ya kuchaguliwa miongoni mwa wapelelezi 12 waliotumwa kuipeleleza nchi ya Kanaani zoezi la upelelezi lilichukua siku 40, waliporejea walitoa taarifa kwa Musa nao walikiri kuwa inchi ile kweli ilikuwa ni nchi njema na ni kweli ilikuwa ni nchi ya maziwa na asali, na miji yake ilikuwa ni mikubwa na yenye ngome na watu wake walikuwa hodari lakini pia waliwaona wana wa Anaki, aidha pia walifanikiwa kuja na vishada vikubwa vya zabibu kutoka nchi ya Mkanaani.

Hesabu 13:27-28 “Wakaenda wakafika kwa Musa, na kwa Haruni, na kwa mkutano wote wa wana wa Israeli, katika jangwa la Parani, huko Kadeshi; wakawaletea habari, wao na mkutano wote, wakawaonyesha matunda ya nchi. Wakamwambia wakasema, Tulifika nchi ile uliyotutuma, na hakika yake, ni nchi yenye wingi wa maziwa na asali, na haya ndiyo matunda yake. Lakini watu wanaokaa katika nchi ile ni hodari, na miji yao ina maboma, nayo ni makubwa sana; na pamoja na hayo tuliwaona wana wa Anaki huko. Amaleki anakaa katika nchi ya Negebu; na Mhiti, na Myebusi, na Mwamori wanakaa katika milima, na Mkanaani anakaa karibu na bahari; na kando ya ukingo wa Yordani.”                

Hata hivyo katika namna ya kushangaza sana taarifa hii iliwatisha baadhi ya wana wa Israel wasiokuwa thabiti katika imani, kwani wao badala ya kuona fursa waliogopa na kufadhaika sana  na kwa mawazo yao walikimbilia kunung’unika na kulalamika badala ya kumuamini Mungu kwamba anaweza kuwarithisha nchi ile kama alivyowaahidi, wapelelezi wengine 10, walikazia kuwa haiwezekani kuirithi inchi ile kwa sababu zao za mitazamo ya kibinadamu, Lakini Kalebu na Yoshua wao walikuwa na mtazamo tofauti kwani walirarua nguo zao na kuwatia moyo watu Kuwa hawapaswi kuogopa kwani Mungu ni mwaminifu na angewapa nchi ile na watu wale walikuwa ni kama chakula kwao.

Hesabu 13:31-33 “Kalebu akawatuliza watu mbele ya Musa, akasema, Na tupande mara, tukaitamalaki; maana twaweza kushinda bila shaka. Bali wale watu waliopanda pamoja naye wakasema, Hatuwezi kupanda tupigane na watu hawa; kwa maana wana nguvu kuliko sisi. Wakawaletea wana wa Israeli habari mbaya ya ile nchi waliyoipeleleza, wakasema, Ile nchi tuliyopita kati yake ili kuipeleleza, ni nchi inayowala watu wanaoikaa; na watu wote tuliowaona ndani yake ni watu warefu mno. Kisha, huko tuliwaona Wanefili, wana wa Anaki, waliotoka kwa hao Wanefili; tukajiona nafsi zetu kuwa kama mapanzi; nao ndivyo walivyotuona sisi.”                

Hesabu 14:6-9 “Na Yoshua mwana wa Nuni, na Kalebu mwana wa Yefune, waliokuwa miongoni mwao walioipeleleza nchi, wakararua nguo zao; wakanena na mkutano wote wa wana wa Israeli wakasema, Nchi ile tuliyopita kati yake ili kuipeleleza, ni nchi njema mno ya ajabu. Ikiwa Bwana anatufurahia, atatuingiza katika nchi hii atupe iwe yetu, nayo ni nchi yenye wingi wa maziwa na asali. Lakini msimwasi Bwana, wala msiwaogope wale wenyeji wa nchi, maana wao ni chakula kwetu; uvuli uliokuwa juu yao umeondolewa, naye Bwana yu pamoja nasi; msiwaogope.”

Kutokana na ujasiri wa Kalebu mwana wa Yefune na Yoshua mwana wa Nuni ambao walionyesha ujasiri mkubwa uliochangiwa na uaminifu wao na imani yao kwa Mungu, Mungu aliapa kuwaangamiza wengine waliolalamika na kunung’unika lakini aliahidi kuwa sivyo itakavyokuwa kwa Kalebu na Yoshua kwa kuwa wao walikuwa na kitu cha ziada na cha tofauti na hivi ndo walivyokua:-

-          Alimfuata Bwana kwa moyo wake wote – Hesabu 14:23-24 “hakika yangu hawataiona hiyo nchi niliyowaapia baba zao, wala katika hao wote walionidharau hapana atakayeiona; lakini mtumishi wangu Kalebu, kwa kuwa alikuwa na roho nyingine ndani yake, naye AMENIANDAMA KWA MOYO WOTE, nitamleta yeye mpaka nchi hiyo aliyoingia; na uzao wake wataimiliki.”

 

Neno ameniandama kwa moyo wote katika maandiko ya kiebrania linasomeka kama ‘achr Rûach ambalo kwa kiingereza ni wind by resemblance yaani amekuwa na roho ya kufanana nami au punzi inayonifanania, maana yake Kalebu alikuwa anaona mambo sawasawa na jinsi Mungu anavyoona, wakati watu wengine wote wanaona mambo hayawezekani Kalebu na Yoshua wao walikuwa wanaona mbona inawezekana, Mungu alimuahidi Kalebu inchi ile kuwa atairithi yeye na watoto wake kwa sababu aliona kama Mungu anavyoona, aliona yasiyowezekana kibinadamu yanawezekana kwa Mungu, alikuwa na mtazamo wa yanayowezekana  wakati wanadamu wakiona yasiyowezekana.

               

-          Walimfuata Bwana kwa kila neno – Kumbukumbu 1:34-36 “Bwana akaisikia sauti ya maneno yenu, akaghadhibika, akaapa, akasema, Hakika yangu hapana mmoja miongoni mwa watu hawa wa kizazi hiki kibaya atakayeiona nchi hiyo nzuri, niliyowaapia baba zenu kuwapa,isipokuwa Kalebu mwana wa Yefune, huyo ataiona; nami nitampa yeye na watoto wake nchi hiyo aliyoikanyaga; KWA KUWA AMEMFUATA BWANA KWA KILA NENO.”

 

Neno amemfuata Bwana kwa kila neno kwenye lugha ya kiebrania linatumika neno Mâlmâlâ ‘Achar ambalo katika kiingereza ni neno Wholly Conjugation au Wholly Conjugate ambalo kwa Kiswahili ni kuenda Sambamba, kufuata barabara, au kufanya au kuungana kwa hiyo sifa nyingine aliyokuwa nayo Kalebu ni kuwa aliungana na Mungu katika neno lake lote, kile kilichozungumzwa na Mungu yeye aliungana nacho kama kilivyosemwa, hakuwa kinyume na neno, alilifuata, alilitenda aliungana nalo na kwa sababu hiyo Mungu anaapa kuwa atairithi nchi. 

 

-          Alimwandama bwana kwa utimilifu – Yoshua 14:13-14 “Yoshua akambarikia, akampa Kalebu, huyo mwana wa Yefune, Hebroni kuwa urithi wake. Kwa hiyo Hebroni ukawa urithi wa Kalebu, mwana wa Yefune, Mkenizi, hata leo; kwa sababu ALIMWANDAMA BWANA, MUNGU WA ISRAELI, KWA UTIMILIFU.”

 

Neno alimuandama kwa utumilifu katika maandiko ya kuiebrania linasomeaka kama Mâlmâlâ kusomeka linasomeka maw-lay kwa kiingereza ni neno concecrate ambalo maana yake kwa utakatifu, kwa unyoofu, kwa kujiweka wakfu, kwa njia tofauti na wengine yaani wakati wengine wanaasi wanazungumza kinyume na ahadi ya Mungu Kalebu yeye alifanya kwa unyoofu kwa utakatifu, kwaajili ya hili Mungu alimpa ahadi, Kalebu hafuati mkumbo             

 

-          Walikuwa na roho nyingine – Hesabu 14:22-24 “kwa sababu watu hawa wote, ambao wameuona utukufu wangu na ishara zangu, nilizozitenda huko Misri, na huko jangwani, pamoja na haya wamenijaribu mara hizi kumi, wala hawakuisikiza sauti yangu; hakika yangu hawataiona hiyo nchi niliyowaapia baba zao, wala katika hao wote walionidharau hapana atakayeiona; lakini mtumishi wangu Kalebu, KWA KUWA ALIKUWA NA ROHO NYINGINE ndani yake, naye ameniandama kwa moyo wote, nitamleta yeye mpaka nchi hiyo aliyoingia; na uzao wake wataimiliki.”

 

Neno alikuwa na roho nyingine katika maandiko ya kiebrania linasomeka kama Achr rûach ambayo kwa kiingereza “Strange Spirit”, roho nyingine, yaani tofauti na wengine ambao walikuwa na roho ya hofu, roho ya woga, yeye alikuwa na Roho Nyingine roho ambayo sio ya kibinadamu, Roho kama ya Mungu, ukiwa na roho nyingine tofauti na wanadamu wa kawaida wewe unakuwa na mtazamo mwingine, mtazamo wa tofauti, unaona kwa jinsi nyingine na kutazama mambo kwa jicho lingine, jicho la kigeni.

Basi sasa unipe mlima huu

Kalebu huyu ambaye hakuwa mtu wa kawaida na alikuwa na kitu cha ziada, akiwa na roho ya kufanana na Mungu, akiwa na moyo wa unyoofu, akiwa anaungana na neno la Mungu, akiwa na roho nyingine tofauti na wayahudi wengine yeye sasa anaidai nchi ya Kanaani aliyoahidiwa na Mungu na anamkumbusha Yoshua kwamba sasa ni wakati wa kupewa urithi wake, na kwa vile Yoshua alikuwepo anamkumbusha yale yote Mungu aliyokuwa ameahidi kwa kinywa cha mtumishi wake Musa, mbele ya Yoshua walipokuwa pamoja naye ni miaka 45 imepita sasa ahadi ilitolewa alipokuwa na miaka 40 sasa anakumbushia kile alichoahidiwa na Mungu, na hataki bure anasema yuko tayari kupigana kwaajili ya ardhi ile tena pale pale wanapoishi majitu yaani wana wa Anaki hili ni jambo la kushangaza sana

Yoshua 14:6-13 Wakati huo wana wa Yuda walimkaribia Yoshua hapo Gilgali; na Kalebu, mwana wa Yefune, huyo Mkenizi, akamwambia, Wewe wajua hilo neno Bwana alilomwambia Musa, huyo mtu wa Mungu, katika habari zangu, na katika habari zako wewe, tulipokuwa katika Kadesh-barnea. Mimi nilikuwa mtu wa miaka arobaini umri wangu, hapo Musa mtumishi wa Bwana aliponituma niende kutoka Kadesh-barnea ili kuipeleleza hiyo nchi; nami nilimletea habari tena, kama ilivyokuwa ndani ya moyo wangu. Lakini wale ndugu zangu waliokwea kwenda pamoja nami waliiyeyusha mioyo ya watu; ila mimi nilimfuata Bwana, Mungu wangu, kwa utimilifu. Kisha Musa akaniapia siku hiyo, akasema, Hakika hiyo nchi ambayo miguu yako imekanyaga itakuwa ni urithi kwako wewe, na kwa watoto wako milele, kwa sababu wewe umemfuata Bwana, Mungu wako, kwa utimilifu. Sasa basi, angalia, yeye Bwana ameniweka hai, kama alivyosema, miaka hii arobaini na mitano, tangu wakati huo Bwana alipomwambia Musa neno hilo, wakati Israeli waliokuwa wakienenda barani; na sasa tazama, hivi leo nimepata miaka themanini na mitano umri wangu. Hata sasa mimi nina nguvu zangu hivi leo kama nilivyokuwa siku hiyo Musa aliyonituma; kama nguvu zangu zilivyokuwa wakati huo, na nguvu zangu ndivyo zilivyo sasa, kwa vita na kwa kutoka nje na kuingia ndani. Basi sasa unipe mlima huu, ambao Bwana alinena habari zake siku hiyo; kwani wewe ulisikia siku hiyo jinsi Waanaki walivyokuwa huko, na miji ilivyokuwa mikubwa yenye boma; yumkini yeye Bwana atakuwa pamoja nami, nami nitawafukuza watoke nje, kama Bwana alivyonena. Yoshua akambarikia, akampa Kalebu, huyo mwana wa Yefune, Hebroni kuwa urithi wake.Kwa hiyo Hebroni ukawa urithi wa Kalebu, mwana wa Yefune, Mkenizi, hata leo; kwa sababu alimwandama Bwana, Mungu wa Israeli, kwa utimilifu. Basi jina la Hebroni hapo kwanza uliitwa Kiriath-arba; huyo Arba alikuwa ni mtu mkubwa kupita wenziwe wote katika hao Waanaki. Hiyo nchi nayo ikatulia, vita vikakoma.”

Miaka mingi imepita lakini Kalebu bado yuko vile vile hakuna kuchuja, nguvu zake ziko vile vile na anataka ardhi na kama ilivyo kawaida ya wanadamu wengi sio rahisi sana kuona faida za kukaa mlimani, tunapenda nchi tambarare iliyonyooka, watu wengi hawapendi milima, na zaidi ya yote mlima huu ulikuwa unamilikiwa na majitu makubwa wana wa Anaki, katika namna ya kushangaza sana Kalebu yeye anautaka mlima huo na yuko tayari kuupigania imani yake haijapoa miaka 45 imepita yeye yuko vile vile, moyo wake uko vile vile anamuamini Mungu vile vile akiwa na nguvu zile zile, akiwa na ujasiri ule ule hajachoka katika mapambano hii inatufundisha kitu kikubwa sana.

Hebroni ilikuwa ni safu ya milima katika milima ya uyahudi kusini mwa Yudea,  ambako ni ukanda wa Magharibi leo, mji wa Hebroni ni moja ya mji unaoheshimika sana na wayahudi kama moja ya miji mitakatifu walikozikwa wazee wetu Ibrahim, Isaka na Yakobo katika pango la Makpela  kwa hiyo ni eneo zuri kihistoria, wakati wa Yoshua sasa eneo hilo lilikaliwa na majitu, lakini Kalebu alikuwa anaiona fursa katika mlima aliouomba kuliko nchi tambarare, kiusalama na kiulinzi yeye angeishi juu na kama askari angeweza kuwaona adui kwa mbali na kuwa salama, chini ya milima kulikua na bonde zuri ambalo lingeweza kufaa kwa kilimo na mifugo na juu ya mlima makazi salama, sasa Kalebu anataka hilo, Kalebu mtazamo wake ni wa tofauti, ni kama ana moyo wa kufanya mambo kwa njia tofauti, ni kama mtu anayesema wakati watu wanaogopa kuendesha ndege mimi nitaendesha, ni kama mtu anayesema wakati watu wanaogopa hisabati mimi ninapenda hisabati, ni kama mtu anayesema wakati watu wanaogopa masomo ya sayansi mimi nitachukua sayansi, Moyo wa Kalebu ni moyo usioogopa mambo magumu, unaona fursa katika mambo yasiyowezekana hauchagui mambo mepesi, unachagua mambo magumu, unaona fursa katika mambo magumu, unawaza na kuyataja yanayoonekana hayawezekani kuwa yanawezekana “BASI SASA UNIPE MLIMA HUU” haijalishi umri umekwenda kiasi gani anataka MLIMA HUU ni mzee lakini bado anawaza na kufikiri akiona maono kama kijana tu, hasemi umri wangu umeenda, hasemi nguvu zangu zimeisha, ametunza Imani yake na uwepo wake vilevile, Kalebu hapoi wala haboi, mtazamo wake kuhusu Mungu uko vilevile wakati makanisa mengi yanapoa yanapofikia umri wa miaka 40, wakati wakristo wengi wanapoa wanapokaa sana katika wokovu, Kalebu hapoi, Kalebu bado anaona maono, Kalebu bado ana ndoto Kalebu bado anamuamini Mungu, haoni kuwa Mungu amechelewa, wala hana muda wa kumlaumu Mungu, anakumbushia haki zake, yuko tayari kwa mapambano, Kalebu hachoki mikesha, Kalebu hachoki kufunga, Kalebu hachoki kuomba, Kalebu hachoki mikutano ya injili, Kalebu hachoki kuhubiri vijijini, Kalebu  hachoki kufungua makanisa, Kalebu hachoki kusoma, Kalebu hachoki kujitoa, Kalebu hachoki kuishi maisha matakatifu, Kalebu hachoki kulifuata neno, Kalebu hachoki kuwa na roho ile ile ya Mungu, Kalebu hachoki kunena kwa lugha, Kalebu ana ujasiri ule ule wa kuhubiri sokoni, Kalebu, ana moto uleule aliokuwa nao jangwani, Kalebu hachoki kuvumilia, Kalebu hachoki kusubiria, Kalebu hachoki majaribu Kalebu hataki kuweka silaha chini Kalebu Kalebu Kalebu una miaka 85 sasa umezeeka, nguvu zako zimeisha, umestaafu sasa Kalebu si utulie, Kalebu si nikutafutie eneo tambarare, Kalebu si ukae karibu na mimi? Kalebu anasema BASI SASA UNIPE MLIMA HUU Mungu wangu ni moyo wa namna gani huu Kalebu? Umepigana vita vingi Kalebu, ukae chini utulie ule mema ya nchi inatosha sasa Kalebu, Kalebu “BASI SASA UNIPE MLIMA HUU” kuna waanaki huko Kalebu, Kalebu nitawafukuza huko, Bwana atakuwa pamoja nami, nguvu zangu hazijapungua niko vilevile kama hapo Musa aliponiapia “BASI SASA UNIPE MLIMA HUU” “shakarabashata skarabatulabosolitasaka Kalebu sotoribakarashika sata rakata risatika yekresatabsoliboso rokosotoka sebetaolasiotifaBASI SASA UNIPE MLIMA HUU neno la Mungu linasema “KWA HIYO HEBRONI UKAWA URITHI WA KALEBU, MWANA WA YEFUNE, MKENIZI, HATA LEO

Mambo ya kujifunza kutoka kwa Kalebu.

-          Ni lazima tuwe na Imani thabiti kwa ahadi za Mungu  -  Kalebu alikuwa ni mtu wa imani na hakuwahi kuchoka katika kumuamini Mungu ni miaka 45 imepita tangu alipokuja kuichunguza na kuipeleleza nchi na hata ingawaje wapelelezi wengine walileta habari chochezi kinyume na imani Kalebu tangu wakati ule aliamini kuwa Mungu hawezi kuwaangusha anakumbuka ahadi za Mungu na hakua na lawama kuwa Mungu amechelewa  au amekawia anaendelea kuipigania haki yake sawa na jinsi na namna ile ile aliyokuwa nayo awali.

 

Yoshua 14:9-12 “Kisha Musa akaniapia siku hiyo, akasema, Hakika hiyo nchi ambayo miguu yako imekanyaga itakuwa ni urithi kwako wewe, na kwa watoto wako milele, kwa sababu wewe umemfuata Bwana, Mungu wako, kwa utimilifu. Sasa basi, angalia, yeye Bwana ameniweka hai, kama alivyosema, miaka hii arobaini na mitano, tangu wakati huo Bwana alipomwambia Musa neno hilo, wakati Israeli waliokuwa wakienenda barani; na sasa tazama, hivi leo nimepata miaka themanini na mitano umri wangu. Hata sasa mimi nina nguvu zangu hivi leo kama nilivyokuwa siku hiyo Musa aliyonituma; kama nguvu zangu zilivyokuwa wakati huo, na nguvu zangu ndivyo zilivyo sasa, kwa vita na kwa kutoka nje na kuingia ndani. Basi sasa unipe mlima huu, ambao Bwana alinena habari zake siku hiyo; kwani wewe ulisikia siku hiyo jinsi Waanaki walivyokuwa huko, na miji ilivyokuwa mikubwa yenye boma; yumkini yeye Bwana atakuwa pamoja nami, nami nitawafukuza watoke nje, kama Bwana alivyonena.”                

 

Kalebu ni moja ya mashujaa wa Imani aliyeweza kusubiria ahadi ya Mungu kwa muda mrefu bila kukata tamaa, wakati Ibrahimu alimsubiri Isaka kwa miaka kama 25 hivi, na Daudi alisubiria ufalme kwa miaka kama 20, Yakobo alivumilia kwa mjomba wake kwa miaka 20 lakini Kalebu alivumilia kwa zaidi ya miaka 45 je wewe ni mvumilivu kwa kiasi gani?

 

-          Kuwa tayari kukabiliana na changamoto – Kalebu alikuwa na ujasiri wa hali ya juu, hakuiomba Hebroni hivi hivi tu, Hebroni ulikuwa ni mlima na sio tambarare na zaidi ya yote ulikuwa unamilikiwa na wana wa Anaki ambao kimsingi walikuwa ni majitu, wale wale walioogopewa na wengine Yeye Kalebu hakuogopa alikuwa tayari kukabiliana na hali hiyo huku akimtegemea Mungu kwamba angekuwa pamoja naye akiamini kuwa atawafukuza.

 

Yoshua 14:12 “Basi sasa unipe mlima huu, ambao Bwana alinena habari zake siku hiyo; kwani wewe ulisikia siku hiyo jinsi Waanaki walivyokuwa huko, na miji ilivyokuwa mikubwa yenye boma; yumkini yeye Bwana atakuwa pamoja nami, nami nitawafukuza watoke nje, kama Bwana alivyonena.”

 

-          Hakuogopa umri wake – Kalebu alikuwa mvumilivu sana na alikuwa na nguvu amefikisha miaka 85 lakini anajisikia ndani yuko vile vile na uwezo ule ule wa kukabiliana na changamoto zile zile alikuwa ni mbobezi katika maswala ya vita na jeshi, jangwa lilikuwa limemuimarisha na kumfanya kuwa mtu mgumu, umri kwake haukuwa kikwazo cha kuzirithi ahadi za Mungu na kuzipambania aliendelea kuwa na maono na imani na matumaini.

 

Yoshua 14:11 “Hata sasa mimi nina nguvu zangu hivi leo kama nilivyokuwa siku hiyo Musa aliyonituma; kama nguvu zangu zilivyokuwa wakati huo, na nguvu zangu ndivyo zilivyo sasa, kwa vita na kwa kutoka nje na kuingia ndani.”

 

-          Aliendelea kuwa mwainifu siku zote – Kwa kweli maneno ya Kalebu yanaonyesha kuwa alikuwa mwaminifu na aliendelea kuwa vile vile mpaka mwisho, uaminifu wake kwa Mungu tangu ujana wake  mpaka wakati huu anaonekana kuwa alikuwa mtu asiyekata tamaa, shujaa na mtu aliyeendelea kumtegemea Mungu huku akikumbuka ahadi zake na haki yake aliudai mlima huo kwa sababu alikuwa na uhakika na Mungu wake kuwa hatomwangusha

 

Yoshua 14:7-8 “Mimi nilikuwa mtu wa miaka arobaini umri wangu, hapo Musa mtumishi wa Bwana aliponituma niende kutoka Kadesh-barnea ili kuipeleleza hiyo nchi; nami nilimletea habari tena, kama ilivyokuwa ndani ya moyo wangu. Lakini wale ndugu zangu waliokwea kwenda pamoja nami waliiyeyusha mioyo ya watu; ila mimi nilimfuata Bwana, Mungu wangu, kwa utimilifu.”   

       

Hitimisho:

Kalebu anampa somo kila mmoja wetu kuhusu imani, uvumilivu, subira, ujasiri, na uaminifu kwa Mungu, alikuwa ni mtu asiyeogopa changamoto wala mtu wa kukata tamaa, hakukuwa na hata tone la hofu maishani mwake kauli yake BASI SASA UNIPE MLIMA HUU iwe changamoto kwetu kwamba tuteendelea kumuamini Mungu sio kwa mambo mepesi tu bali hata kwa mambo magumu, na tutaendelea kuwa wavumilivu bila kujali muda, na tutaendelea katika imani bila kupoa, na tutaendelea kuwa na ujasiri wa kukabiliana na magumu bila kujali umri na kuwa tayari kumtumikia Mungu mpaka siku zetu za mwisho!

 

Rev. Innocent Samuel Kamote

Mkuu wa wajenzi mwenye Hekima!