Mathayo 27:50-54 “Naye Yesu akiisha kupaza
sauti tena kwa nguvu, akaitoa roho yake. Na tazama, pazia la hekalu likapasuka
vipande viwili toka juu hata chini; nchi ikatetemeka; miamba ikapasuka;
makaburi yakafunuka; ikainuka miili mingi ya watakatifu waliolala; nao wakiisha
kutoka makaburini mwao, baada ya kufufuka kwake, wakauingia mji mtakatifu,
wakawatokea wengi. Basi yule akida, na hao waliokuwa pamoja naye wakimlinda
Yesu, walipoliona tetemeko la nchi na mambo yaliyofanyika, wakaogopa sana,
wakisema, Hakika huyu alikuwa Mwana wa Mungu.”
Utangulizi:
Mojawapo ya matukio makubwa ya
kutisha na kushangaza yaliyoambatana na kifo cha Bwana wetu Yesu Kristo pale
Msalabani ni pamoja na tukio la kupasuka kwa pazia la hekalu, tukio hili lina
tupa ishara madhubuti juu ya umuhimu wa kifo cha Yesu Kristo na nguvu ya
upatanisho iliyofanywa na kifo chake kwa wanadamu wote wakiwemo Wayahudi pia,
Njia ya kuufikia uwepo wa Mungu ilikuwa sio rahisi wakati wa agano la kale na
ni watu wachache sana waliokuwa na ruhusa ya kuukaribia uwepo wa Mungu. Pazia
kubwa zito lilitenganisha mahali patakatifu sana palipokuwa na kiti cha rehema
na uwepo wa watu wa kawaida hivyo kuwanyima watu fursa ya kukutana na Mungu
bila mtu wa kuingilia kati. Pazia hili lilitengenezwa kwa maelekezo ya Mungu
kwa Musa, likizuia eneo la Sanduku.
Kutoka 26:30-33 “Nawe utaisimamisha hiyo
maskani sawasawa na mfano wake ulioonyeshwa mlimani. Nawe fanya pazia la nyuzi
za rangi ya samawi, na za rangi ya zambarau, na za rangi nyekundu, na nguo za
kitani nzuri zenye kusokotwa, litafumwa na kutiwa makerubi, kazi ya fundi
stadi; kisha litungike katika nguzo nne za mti wa mshita zilizofunikwa dhahabu,
vifungo vyake vitakuwa vya dhahabu, katika matako ya fedha manne. Nawe tungika
lile pazia chini ya vile vifungo, nawe lete lile sanduku la ushuhuda na kulitia
humo nyuma ya pazia; na lile pazia litawagawanyia kati ya patakatifu, na mahali
patakatifu sana.”
Leo tutachukua muda kiasi
kujifunza umuhimu wa pazia hili kupasuka wakati wa kifo cha Yesu Kristo na
maana yake kubwa sana kwetu ambayo kimsingi inatupa tiketi ya kuuendea uwepo wa
Mungu na kuufurahia ushirika na Mungu bila kupata madhara ya aina yoyote na
bila ya kupitia kwa mtu yeyote, tutajifunza somo hili, Na tazama, Pazia la
hekalu likapasuka kwa kuzingatia vipengele vikuu vitatu vifuatavyo:-
·
Kazi ya
Pazia la hekalu.
·
Na tazama
pazia la hekalu likapasuka.
·
Faida za
kupasuka kwa pazia la hekalu.
Kazi ya pazia la Hekalu!
Pazia la Hekalu ilikuwa ni nguo
maalumu iliyotengenezwa kwa nyuzi za kitani zilizofumwa kwa ustadi kwa rangi
mchangayiko wa aina tatu, rangi ya samawi, yaani mbingu, rangi ya zambarau na
nyekundu, Pazia hili lilikuwa na ukubwa kwa maana ya urefu wa futi sitini (Sawa
na mita 18) na upana wa futi 30 (sawa na mita 9) na unene wake ulikuwa kati ya
inchi 4 mpaka sita yaani kati ya sentimita 10-15. Aidha lilifumwa pia likiwa na
picha ya makerubi mfano wa ulinzi kwaajili ya patakatifu pa patakatifu, Pazia
hili lilikuwa na kazi ya kupafunika au kutenganisha mahali patakatifu na
patakatifu sana. Pazia hili lilitengenezwa kwa ustadi kufuata maelekezo
yaliyotolewa na Mungu.
Kutoka 36:35-38 “Kisha akafanya hilo pazia
la nyuzi za rangi ya samawi, na za rangi ya zambarau, na nyekundu, na kitani
nzuri zilizosokotwa; akatia na makerubi kazi ya fundi stadi, ndivyo
alivyofanya. Naye akafanya kwa ajili yake nguzo nne za mti wa mshita,
akazifunika dhahabu; na kulabu zake zilikuwa za dhahabu; naye akasubu kwa ajili
yake matako manne ya fedha. Kisha akafanya pazia la sitara kwa ajili ya mlango
wa Hema, la nguo ya rangi ya samawi, na ya rangi ya zambarau, na nyekundu, na
nguo ya kitani nzuri ya kusokotwa, kazi ya mwenye kutia taraza, na nguzo zake
tano pamoja na kulabu zake; naye akavifunika dhahabu vichwa vyake na vifungo
vyake; na matako yake matano yalikuwa ya shaba.”
Kazi kubwa ya Pazia hili ilikuwa
ni kutenganisha mahali patakatifu na patakatifu sana, hekalu lilikuwa na sehemu
kubwa tatu, Patakatifu sana au patakatifu pa patakatifu mahali ambapo lilikaa
sanduku la agano la Bwana, na patakatifu mahali ambapo palikuwa na madhabahu ya dhahabu ya kufukizia uvumba, taa
ya vinara saba na meza ya mikate ya wonyesho, eneo hili kuhani aliingia
kwaajili ya kufukiza uvumba, kila siku na kisha eneo la tatu ulikuwa ni uwa wa kawaida
ambapo Wayahudi walikaa, na Mataifa wasio Wayahudi walikaa mbali zaidi katika uwa
wa wamataifa. Pazia lilitenganisha mahali lilipokuwepo sanduku la agano ambalo
juu yake kulikuwa na kiti cha rehema,
mahali hapa kuhani mkuu aliingia mara moja tu kwa mwaka kufanya
upatanisho kwa watu na Mungu, siku ya upatanisho tena akiwa amejitakasa kweli
kweli (siku saba maalumu kabla ya kuingia katika ibada hiyo), Pazia hili ni
alama ikiwa na fundisho kuwa Mungu ni MTAKATIFU
SANA na sio rahisi mwanadamu wa kawaida kumsogelea bila kupata madhara,
Pazia hili zito lilikuwa ni katazo kuwa huwezi kuufikia uwepo wa Mungu wala
kuona ukawa salama, Kuhani mkuu mwenyewe aliingia hapa mara moja kwa mwaka wala
si pasipo damu tena siku ya upatanisho (Yom
Kippur) kutoa dhabihu ya dhambi kwaajili yake, familia yake na watu wa taifa zima! Kinyume chake kifo
kingehusika.
Kutoka 30:10 “Naye Haruni atafanya
upatanisho juu ya pembe zake mara moja kila mwaka; kwa damu ya ile sadaka ya
dhambi ya kufanya upatanisho, mara moja kila mwaka ataifanyia upatanisho,
katika vizazi vyenu vyote; ni takatifu sana kwa BWANA.”
Waebrania 9:1-9 “Basi hata agano la kwanza
lilikuwa na kawaida za ibada, na patakatifu pake, pa kidunia. Maana hema
ilitengenezwa, ile ya kwanza, mlimokuwa na kinara cha taa, na meza, na mikate
ya Wonyesho; ndipo palipoitwa, Patakatifu. Na nyuma ya pazia la pili, ile hema
iitwayo Patakatifu pa patakatifu, yenye chetezo cha dhahabu, na sanduku la
agano lililofunikwa kwa dhahabu pande zote, mlimokuwa na kopo la dhahabu lenye
ile mana, na ile fimbo ya Haruni iliyochipuka, na vile vibao vya agano; na juu
yake makerubi ya utukufu, yakikitia kivuli kiti cha rehema; basi hatuna nafasi
sasa ya kueleza habari za vitu hivi kimoja kimoja. Basi, vitu hivi vikiisha
kutengenezwa hivyo, makuhani huingia katika hema hiyo ya kwanza daima,
wakiyatimiza mambo ya ibada. Lakini katika hema hiyo ya pili kuhani mkuu
huingia peke yake, mara moja kila mwaka; wala si pasipo damu, atoayo kwa ajili
ya nafsi yake na kwa dhambi za kutokujua za hao watu. Roho Mtakatifu akionyesha
neno hili, ya kwamba njia ya kupaingia patakatifu ilikuwa haijadhihirishwa
bado, hapo hema ya kwanza ilipokuwa ingali ikisimama; ambayo ndiyo mfano wa
wakati huu uliopo sasa; wakati huo sadaka na dhabihu zinatolewa, zisizoweza kwa
jinsi ya dhambi kumkamilisha mtu aabuduye,”
Kwa sababu hii watu wa kawaida
hawakuweza kabisa kupakaribia mahali hapa, kwani hata kuhani alivalishwa
kengele (njuga) maalumu kiunoni na mguuni na kufungwa kamba maalumu ili kama
atapigwa na Mungu na kufa wamvute nje, watu wengine wote, wangekuwa nje mbali
wakiwa wametengwa mbali na mahali hapo patakatifu sana kwaajili ya dhambi na
matakwa ya kisheria, hivyo pazia lilikuwa linawakilisha ugumu wa kuufikia uwepo
wa Mungu, Pazia lilikuwa linawakumbusha wakati wote kuwa Mungu ni MTAKATIFU SANA na sisi wengine wote
hatustahili, dhambi ilikuwa imetufarakanisha mbali na Mungu na hakuna jitihada
yoyote ya kibinadamu inayoweza kutuunganisha, utaratibu wote huu ulikuwa pia
unafundisha ya kwamba tunahitaji mtu wa kutupatanisha na Mungu, hakuna
mwanadamu yeyote aliruhusiwa kupita kwenye pazia hili, maovu ya mwanadamu
yalimfarikisha na Mungu.
Isaya 59:1-2 “Tazama, mkono wa Bwana
haukupunguka, hata usiweze kuokoa wala sikio lake si zito, hata lisiweze
kusikia; lakini maovu yenu yamewafarikisha ninyi na Mungu wenu, na dhambi zenu
zimeuficha uso wake msiuone, hata hataki kusikia.”
Na tazama pazia la hekalu likapasuka.
Katika namna ya kushangaza sana
na isiyoweza kubuniwa kibinadamu Neno la Mungu katika agano jipya
linatufahamisha katika injili zifafanazo zote kuwa pazia hili lililokuwa na
unene wa nchi 4-6 hivi kwa njia ya muujiza mkubwa usiokuwa wa kibinadamu mara
Yesu alipokata roho na kufa msalabani pazia hili la hekalu lilipasuka katikati
vipande viwili kutoka juu hata chini! Muujiza huu usiokuwa wa kawaida
ulirekodiwa katika injili zote tatu zifananazo.
Mathayo 27:50-51. “Naye Yesu akiisha kupaza
sauti tena kwa nguvu, akaitoa roho yake. Na tazama, pazia la hekalu likapasuka
vipande viwili toka juu hata chini; nchi ikatetemeka; miamba ikapasuka;”
Marko 15:37-38 “Naye Yesu akatoa sauti kuu,
akakata roho. Pazia la hekalu likapasuka vipande viwili toka juu hata chini.”
Luka 23:44-45 “Hapo ilikuwa yapata saa
sita, kukawa giza juu ya nchi yote hata saa kenda, jua limepungua nuru yake;
pazia la hekalu likapasuka katikati.”
Kwa nini tukio hili linakuwa la
muhimu kiasi hiki mpaka kila mtume anarekodi habari hii, kwa ujumla hili sio
jambo dogo, lina kitu cha muhimu cha kutufundisha, Mwandishi wa kitabu cha Waebrania
anaeleza kwamba sababu kubwa ni kuwa Yesu Kristo mwana wa Mungu alifanyika
Mwana kondoo mkamilifu, aliyejitoa mwenyewe kama sadaka ya kudumu ya milele na
kwa damu yake kuwa mpatanishi kati ya Mungu na wanadamu, Mwandishi anafafanua
kuwa lile pazia linawakilisha mwili wa Yesu Kristo, kwa hiyo wakati mwili ule
unasulubiwa kwa ajili ya dhambi zetu, Kristo anafanyika kuwa mpatanishi kati ya
Mungu na wanadamu na hivyo hatuhitaji tena kuhani wa kuingia katika kiti cha
rehema kwaajili yetu, na ukuta uliotutenganisha na Mungu umebomolewa,
kusulubiwa kwa Yesu Kristo kumeleta uponyaji mkubwa sana kwetu wa kimwili na
kiroho, na hatuhitaji tena mtu awaye yote ajifanye “dalali” wa kiroho, au
ajifanye kuwa yeye anaweza kutupatanisha
na Mungu ni ukweli ulio wazi kuwa mpatanishi ni mmoja tu. Yesu Kristo!
Waebrania 10:19-21 “Basi, ndugu, kwa kuwa
tuna ujasiri wa kupaingia patakatifu kwa damu ya Yesu, njia ile aliyotuanzia
iliyo mpya, iliyo hai, ipitayo katika pazia, yaani, mwili wake; na kuwa na
kuhani mkuu juu ya nyumba ya Mungu;”
Isaya 53:2-5 “Maana alikua mbele zake kama
mche mwororo, Na kama mzizi katika nchi kavu; Yeye hana umbo wala uzuri; Na
tumwonapo hana uzuri hata tumtamani. Alidharauliwa na kukataliwa na watu; Mtu
wa huzuni nyingi, ajuaye sikitiko; Na kama mtu ambaye watu humficha nyuso zao,
Alidharauliwa wala hatukumhesabu kuwa kitu. Hakika ameyachukua masikitiko yetu,
Amejitwika huzuni zetu; Lakini tulimdhania ya kuwa amepigwa, Amepigwa na Mungu,
na kuteswa. Bali alijeruhiwa kwa makosa yetu, Alichubuliwa kwa maovu yetu; Adhabu
ya amani yetu ilikuwa juu yake, Na kwa kupigwa kwake sisi tumepona.”
1Timotheo 2:5-6 “Kwa sababu Mungu ni mmoja,
na mpatanishi kati ya Mungu na wanadamu ni mmoja, Mwanadamu Kristo Yesu; ambaye
alijitoa mwenyewe kuwa ukombozi kwa ajili ya wote, utakaoshuhudiwa kwa majira
yake.”
Waebrania 4:14-16 “Basi, iwapo tunaye
kuhani mkuu aliyeingia katika mbingu, Yesu, Mwana wa Mungu, na tuyashike sana
maungamo yetu. Kwa kuwa hamna kuhani mkuu asiyeweza kuchukuana nasi katika
mambo yetu ya udhaifu; bali yeye alijaribiwa sawasawa na sisi katika mambo
yote, bila kufanya dhambi. Basi na tukikaribie kiti cha neema kwa ujasiri, ili
tupewe rehema, na kupata neema ya kutusaidia wakati wa mahitaji.”
1Petro 2:9-10 “Bali ninyi ni mzao mteule,
ukuhani wa kifalme, taifa takatifu, watu wa milki ya Mungu, mpate kuzitangaza
fadhili zake yeye aliyewaita mtoke gizani mkaingie katika nuru yake ya ajabu;
ninyi mliokuwa kwanza si taifa, bali sasa ni taifa la Mungu; mliokuwa hamkupata
rehema, bali sasa mmepata rehema.”
1Wakorintho 6:19 “Au hamjui ya kuwa mwili
wenu ni hekalu la Roho Mtakatifu aliye ndani yenu, mliyepewa na Mungu? Wala
ninyi si mali yenu wenyewe;”
Faida za kupasuka kwa pazia la hekalu
Kupasuka kwa Pazia la hekalu
kunatupa faida lukuki ambazo muda usingeliweza kutosha kuelezea yote lakini
njia ya kumuendea Mungu na kufanya ushirika naye leo imekuwa wazi kwa kila
aaminiye, kutoka kokote kule duniani!
-
Tunaweza kumuendea Mungu kwa maombi na
kuzungumza naye moja kwa moja bila dalali huku tukiwa na uhakika kuwa Mungu anatusikia
Wafilipi 4:6-7 “Msijisumbue kwa neno lo
lote; bali katika kila neno kwa kusali na kuomba, pamoja na kushukuru, haja
zenu na zijulikane na Mungu. Na amani ya Mungu, ipitayo akili zote,
itawahifadhi mioyo yenu na nia zenu katika Kristo Yesu.”
-
Tunaweza kumuendea kwa ibada na kumuabudu kwa
kumsifu na kumshukuru tukiwa na uhakika kuwa yeye ni Bwana Mungu wetu kwani
tuna uwezo wa kuingia malangoni mwake Zaburi
100:4-5 “Ingieni malangoni mwake kwa kushukuru;
Nyuani mwake kwa kusifu; Mshukuruni, lihimidini jina lake; Kwa kuwa Bwana ndiye
mwema; Rehema zake ni za milele; Na uaminifu wake vizazi na vizazi.”
-
Tunaweza kulifurahia neno lake ambalo kimsingi
zamani ni makuhani pekee ndio waliokuwa na uwezo wa kulisoma na kulifafanua kwa
watu, Neno la Mungu sasa ni kwaajili ya kila mtu na linaeleweka kwa kila
amtafutaye Mungu
2Timotheo 3:16-17 “Kila
andiko, lenye pumzi ya Mungu, lafaa kwa mafundisho, na kwa kuwaonya watu makosa
yao, na kwa kuwaongoza, na kwa kuwaadibisha katika haki; ili mtu wa Mungu awe
kamili, amekamilishwa apate kutenda kila tendo jema.”
-
Tunaweza kuufurahia uwepo wa Mungu pamoja na
wengine kwani kila tunapokutana na kukusanyika kwa jina lake yeye naye
anaungana nasi na kuwa kati kati yetu.
Mathayo 18:18-20 “Amin,
nawaambieni, yo yote mtakayoyafunga duniani yatakuwa yamefungwa mbinguni; na yo
yote mtakayoyafungua duniani yatakuwa yamefunguliwa mbinguni. Tena nawaambia,
ya kwamba wawili wenu watakapopatana duniani katika jambo lo lote
watakaloliomba, watafanyiwa na Baba yangu aliye mbinguni. Kwa kuwa walipo
wawili watatu wamekusanyika kwa jina langu, nami nipo papo hapo katikati yao.”
-
Tunaweza kuziungama dhambi zetu wenyewe moja kwa
moja na Mungu akatusamehe bila kupitia kwa kuhani wa kibinadamu kama ilivyo katika
baadhi ya dini ambapo makuhani hutaka kuwatawala wanadamu na kuwanyanyasa
kisaikolojia kwa sababu wanataka kusikiliza dhambi zao, au wanafanya kazi ya
upelelezi
1Yohana 1:8-9 “Tukisema
kwamba hatuna dhambi, twajidanganya wenyewe, wala kweli haimo mwetu.
Tukiziungama dhambi zetu, Yeye ni mwaminifu na wa haki hata atuondolee dhambi
zetu, na kutusafisha na udhalimu wote.”
Kupasuka kwa pazia la hekalu ni tukio la kusangaza sana na
si la kihistoria tu bali ni kazi kubwa ya Mungu yenye kumaanisha kuwa Mungu
anatoa mwaliko kwa kila mmoja kuukaribia uwepo wake haijalishi umetoka katika
historia gani, na wa kabila gani, Mungu
sasa haishi nyuma ya pazia wala hafikiwi kupitia mtu, kuhani au dalali, lakini
kupitia Bwana wetu Yesu Kristo mlango ulio wazi umefunguliwa kwa jamii nzima ya
aina binadamu duniani kuwa huru na kuufikia uwepo wa Mungu, hakuna wa kujidai
katikati yetu badala yake tunasaidiana na kujengana huku tukitiana moyo kwamba
leo uiamini kazi yake Bwana aliyoifanya
msalabani kwamba imefungua njia kwaajili yako na yangu na Wayahudi wote duniani
kokote waliko kwamba Mungu yuko tayari kukutana na kila mtu anayemjia katika
jina la Yesu Kristo Mwana wa Mungu aliye hai Amen
Na. Rev. Innocent
Samuel Kamote
Mkuu wa wajenzi mwenye Hekima!


.jpg)
