Jumapili, 5 Julai 2026

Kwa kuwa sasa Bwana ametufanyia nafasi!


Mwanzo 26:19-22 “Watumwa wa Isaka wakachimba katika lile bonde, wakapata kisima cha maji yanayobubujika. Wachungaji wa Gerari wakagombana na wachungaji wa Isaka wakisema, Maji haya ni yetu. Ndipo akakiita jina la kile kisima Eseki, kwa sababu waligombana naye. Wakachimba kisima kingine, wakagombania na hicho tena. Akakiita jina lake Sitna. Akaondoka huko akachimba kisima kingine, wala hicho hawakukigombania. Akakiita jina lake Rehobothi, akasema, Kwa kuwa sasa BWANA ametufanyia nafasi, nasi tutazidi katika nchi.”




Utangulizi:

Ni muhimu kufahamu kuwa mtu awaye yote anapokuwa amebarikiwa na Mungu, au kama Mungu yuko pamoja na yeye anaweza kupitia vipingamizi vya aina mbalimbali katika maisha, watu wa Mungu wakati mwingine watapitia chuki zisizokuwa za kawaida, kuonewa wivu, na wakati mwingine kupitia mapambano mengi, Maisha ya Isaka ni mojawapo ya mfano wa matukio kama hayo, baada ya kuwa Mungu amemfungulia milango ya Baraka na uhuru, kutoka katika kuandamwa na vita na chuki na wivu wa maisha kutoka kwa wafilisti, Waligombania na kumpokonya visima vyake viwili yaani maji ya Eseki na Stina, hatimaye alipata maji sehemu nyingine ambapo alipaita Rehoboth akitangaza kwa imani kuwa sasa Bwana amemfanyia nafasi!, kwani kisima hicho hakikugombaniwa tena.

Mwanzo 26:19-22 “Watumwa wa Isaka wakachimba katika lile bonde, wakapata kisima cha maji yanayobubujika. Wachungaji wa Gerari wakagombana na wachungaji wa Isaka wakisema, Maji haya ni yetu. Ndipo akakiita jina la kile kisima Eseki, kwa sababu waligombana naye. Wakachimba kisima kingine, wakagombania na hicho tena. Akakiita jina lake Sitna. Akaondoka huko akachimba kisima kingine, wala hicho hawakukigombania. Akakiita jina lake Rehobothi, akasema, Kwa kuwa sasa BWANA ametufanyia nafasi, nasi tutazidi katika nchi.”

Leo tutachukua muda kujifunza na kutafakari kwa kina kuhusiana na maisha ya Isaka ambayo kimsingi yanatufundisha kuwa maisha ya watu wa Mungu na watu wa kawaida yana changamoto za aina mbalimbali lakini hata hivyo tunapoendelea kumtegemea Mungu hatimaye Mungu hutupa ahueni, tutajifunza somo hili Kwa kuwa sasa Bwana ametufanyia nafasi kwa kuzingatia vipengele muhimu vitatu vifuatayo:-

·         Maana ya maneno Bwana ametufanyia nafasi

·         Maisha ya changamoto za mtu wa Mungu

·         Kwa kuwa sasa Bwana ametufanyia nafasi


Maana ya maneno Bwana ametufanyia nafasi.

Maneno Kwa kuwa Bwana ametufanyia nafasi  kwa Kiebrania “Rehoboth” yalitamkwa na Isaka yakimaanisha majira ya Mungu ya kuwapa watu wake mpenyo, pumziko la kiroho, nafasi ya kukua, nafasi ya kuongezeka, nafasi ya kuwa na Amani, nafasi ya kutokuweko katika migogoro, nafasi ya kustawi pasipokuwa na upinzani, nafasi ya thamani na utulivu, kwa hiyo neno “Rehoboth” au “Rechovoth” la Kiebrania lina maana ya Nafasi kubwa, eneo la kukua na kupanuka, uhuru wa kutenda bila upinzani, nafasi ya kustawi, na nafasi ya kuwa nje ya vikwazo, hali hii haisababishwi na akili za kibinadamu bali inasababishwa na Mungu anapoingilia kati na kundoa shinikizo na msongamano wa changamoto ili kutoa utulivu kwa watu wake, huu ni mchakato wa kuondoka katika mashinikizo kadhaa ya maisha yanayopelekea kuifikia ndoto ya utulivu unaohitajika kibinadamu.

Mungu alimpa nafasi Rehoboth Yusufu baada ya mapito ya muda mrefu katika maisha kwa kusudi la kufikia hatima yake - Mwanzo 41:38-41 “Farao akawaambia watumwa wake, Tupate wapi mtu kama huyu, mwenye roho ya Mungu ndani yake? Farao akamwambia Yusufu, Kwa kuwa Mungu amekufahamisha hayo yote, hapana mwenye akili na hekima kama wewe. Basi wewe utakuwa juu ya nyumba yangu, na kwa neno lako watu wangu watatawaliwa. Katika kiti cha enzi tu nitakuwa mkuu kuliko wewe. Farao akamwambia Yusufu, Tazama, nimekuweka juu ya nchi yote ya Misri.”

Mungu alimpa nafasi Daudi nafasi ya kutoka katika hali duni ya kuchunga kondoo na kudharaulika katika familia mpaka kuwa mfalme katika Israel – 1Samuel 16:11-13 “Kisha Samweli akamwambia Yese, Watoto wako wote wapo hapa? Naye akasema, Amesalia mdogo wao, na tazama, anawachunga kondoo. Basi Samweli akamwambia Yese, Tuma watu, wamlete; kwa sababu hatutaketi hata atakapokuja huku. Basi akatuma mtu, naye akamleta kwao. Naye alikuwa mwekundu, mwenye macho mazuri, na umbo lake lilikuwa la kupendeza. Bwana akasema, Ondoka, umtie mafuta; maana huyu ndiye.Ndipo Samweli akaitwaa pembe yenye mafuta, akamtia mafuta kati ya ndugu zake; na roho ya Bwana ikamjilia Daudi kwa nguvu tangu siku ile. Basi Samweli akaondoka, akaenda zake Rama.”

Mungu anapokufanyia nafasi au kukuletea “Rehoboth” anakuweka katika mahali ambapo adui zako hawawezi kuzuia maendeleo na ustawi wako, Milango iliyokuwa imefungwa au iliyokuwa inakutana na upinzani huanza kufunguka na kupata upenyo, Milango ya Baraka huanza kutiririka kwa urahisi, miguu yako inawekwa mahali palipoinuka na hakuna taabu tena ya kupita katika mabonde

Zaburi 31:7-8 “Na nishangilie, nizifurahie fadhili zako, Kwa kuwa umeyaona mateso yangu. Umeijua nafsi yangu taabuni, Wala hukunitia mikononi mwa adui; Miguu yangu umeisimamisha panapo nafasi.”

Maisha ya changamoto za mtu wa Mungu

Kabla Isaka hajapata utulivu wa maisha “Rehoboth” alipitia changamoto nyingi sana ambazo wakati mwingine hata watu wengine wa Mungu wanapitia, hii inamaanisha kuwa changamoto ni sehemu ya kawaida ya maisha ya mwanadamu lakini hata hivyo tukimtegemea Mungu atajitokeza hatimaye na kutupatia nafasi

·         Isaka alipoteza mama yake mpendwa Sara -  Jambo hili liliumiza sana maisha yake kama wote tunavyofahamu unapoondokewa na wazazi, moyo unauma sana na unagubikwa na upweke mkubwa  hata hivyo ujio wa Rebeka katika maisha ya Isaka ulimpa unafuu katika changamoto hiyo

 

Mwanzo 24:67 “Isaka akamwingiza Rebeka katika hema ya mama yake, Sara, akamtwaa Rebeka, akawa mkewe, akampenda; Isaka akafarijika kwa ajili ya kufa kwa mamake.”

 

·         Isaka alipitia kipindi cha kukosa mtoto miaka 20 – Baada ya Rebeka kuwa faraja kwa muda sasa wanakutana na changamoto nyingine katika maisha na sasa wanakosa mtoto kwa muda wa miaka 20, Isaka alimuoa Rebeka akiwa na miaka 40 na alikuja kupata watoto Esau na Yakobo akiwa na miaka 60, hiki ni kipindi cha kupimwa imani na uvumilivu, na ni mpaka Isaka alipomuomba Mungu ndipo Mungu alipojibu maombi na watoto mapacha wakapatikana

 

Mwanzo 25:19-28 “Na hivi ndivyo vizazi vya Isaka, mwana wa Ibrahimu. Ibrahimu alimzaa Isaka. Isaka akawa mwenye miaka arobaini alipomtwaa Rebeka binti Bethueli, Mshami, wa Padan-aramu, ndugu wa Labani, Mshami, kuwa mke wake. Isaka akamwomba BWANA kwa ajili ya mke wake, maana alikuwa tasa. Naye BWANA akamwitikia, na Rebeka mkewe akachukua mimba. Watoto wakashindana tumboni mwake. Naye akasema, Ikiwa ni hivi, kuishi kwanifaa nini? Akaenda kumwuliza BWANA. BWANA akamwambia, Mataifa mawili yamo tumboni mwako, Na kabila mbili za watu watafarakana tangu tumboni mwako. Kabila moja litakuwa hodari kuliko la pili, Na mkubwa atamtumikia mdogo. Siku zake za kuzaa zilipotimia, tazama! Mapacha walikuwamo tumboni mwake. Wa kwanza akatoka, naye alikuwa mwekundu mwili wote kama vazi la nywele. Wakamwita jina lake Esau. Baadaye ndugu yake akatoka, na mkono wake unamshika Esau kisigino. Akaitwa jina lake Yakobo. Isaka alikuwa mwenye miaka sitini mkewe alipowazaa. Watoto wakakua, Esau alikuwa mtu ajuaye kuwinda wanyama, mtu wa nyikani, na Yakobo alikuwa mtu mtulivu, mwenye kukaa hemani. Basi Isaka akampenda Esau, kwa sababu alikula mawindo yake, na Rebeka akampenda Yakobo.”

 

·         Isaka alikabiliwa na njaa kubwa katika inchi – Akiwa katika nchi ya ahadi Isaka anakumbwa na njaa kali sana, njaa kama ya siku za baba yake Abrahamu ambayo ilimpelekea Abrahamu kukimbilia Misri hata hivyo kwa neema ya Mungu, Mungu alisema na Isaka asishuke kwenda Misri kama ilivyokuwa kwa baba yake, Mungu aliamua kumbariki pale pale  mahali ambapo wengine walikuwa hawana matumaini.

 

Mwanzo 26:1-5 “Ikawa njaa katika nchi hiyo, mbali na njaa ile ya kwanza iliyokuwa siku za Ibrahimu. Isaka akamwendea Abimeleki, mfalme wa Wafilisti, huko Gerari. BWANA akamtokea, akasema, Usishuke kwenda Misri, kaa katika nchi nitakayokuambia. Kaa ugenini katika nchi hiyo, nami nitakuwa pamoja nawe, na kukubariki, maana nitakupa wewe na uzao wako nchi hizi zote. Nami nitakifanya imara kiapo nilichomwapia Ibrahimu baba yako. Nitazidisha uzao wako kama nyota za mbinguni, nami nitawapa uzao wako nchi hizi zote, na katika uzao wako mataifa yote ya dunia watajibarikia. Kwa sababu Ibrahimu alisikia sauti yangu, akayahifadhi maagizo yangu, na amri zangu, na hukumu zangu, na sheria zangu.”

 

·         Isaka alikabiliwa na kuonewa wivu (Husuda) na wafilisti – Mungu alimbariki sana Isaka baada ya kubaki katika inchi ya Mkanaani, Mungu alikuwa amemuwezesha Isaka kuchimba visima vya baba yake Ibrahimu na kumsaidia kwa kutumia maji yanayobubujika kufanya kilimo cha umwagiliaji na kujipatia mazao na kuwanywesha mifugo hivyo kukawa na mafanikio makubwa sana hata wakati wa njaa Isaka alipanda kipimo cha mbegu na kuvuna mara mia, hivyo mtu huyu akawa mkuu mno na hapo ndipo Wafilisti wakamuonea wivu, kumbe kadiri Mungu anavyokubariki sana na kukuinua juu ndivyo Baraka zako zinavyoambatana na upinzani kutoka kwa watu wenye wivu wenye uchungu

 

Mwanzo 26:12-14 “Isaka akapanda mbegu katika nchi ile, akapata mwaka ule vipimo mia kwa kimoja, BWANA akambariki. Na mtu huyu akawa mkuu, akazidi kusitawi, hata akawa mkuu sana. Akawa na mali ya kondoo, na mali ya ng'ombe, na watumwa wengi. Hao Wafilisti wakamhusudu.”

 

·         Isaka alipambana na jaribu la kufukiwa kwa visima vyake – Bila shaka wafilisti walibaini kuwa utajiri wa Isaka na mafanikio makubwa aliyokuwa nayo ni uwepo wa Mungu na vile vile visima alivyokuwa amechimba na vikawa vinabubujisha maji, Wafilisti waliamua kuvifukia  visima  vyote ambavyo kimsingi vilikuwa vya baba yake yaani Abrahamu, Wafilisti walivifukia, wakati wote shetani atataka kufukia kila chanzo cha Baraka kwa watu wa Mungu ili usitoke

 

Mwanzo 26:15-21 “Na vile visima vyote walivyochimba watumwa wa baba yake, siku za Ibrahimu babaye, Wafilisti walikuwa wamevifukia, wakavijaza kifusi. Abimeleki akamwambia Isaka, Utoke kwetu, maana wewe una nguvu sana kuliko sisi. Basi Isaka akatoka huko akapiga kambi katika bonde la Gerari, akakaa huko.Isaka akarudi akavichimbua vile visima vya maji walivyovichimba siku za Ibrahimu babaye; maana wale Wafilisti walikuwa wamevifukia baada ya kufa kwake Ibrahimu; naye akaviita majina kufuata majina alivyoviita babaye.Watumwa wa Isaka wakachimba katika lile bonde, wakapata kisima cha maji yanayobubujika. Wachungaji wa Gerari wakagombana na wachungaji wa Isaka wakisema, Maji haya ni yetu. Ndipo akakiita jina la kile kisima Eseki, kwa sababu waligombana naye. Wakachimba kisima kingine, wakagombania na hicho tena. Akakiita jina lake Sitna.”

 

·         Isaka alifukuzwa kwa sababu ua ukuu wake -  Isaka alibarikiwa sana na kuwa mtu mkubwa sana, uwepo wa Mungu ulikuwa pamoja naye, upako na karama zilikaa juu yake, hakuwa mtu wa vita alikuwa mtu wa utulivu na mtu wa Amani lakini hata hivyo adui zake walishindwa kumstahimili na hivyo waliamua kumfukuza, ziko nyakati ambazo unaweza kukataliwa bila sababu au unaweza kutengenezewa zengwe ili usiwepo katika maeneo hayo na sababu kubwa watu wanadhani ukuu wako unatokana na hapo ulipo, lakini sio hivyo tu watu wema wakati mwingine hukataliwa na hata kuuawa kwa sababu ya wema wao

 

Mwanzo 26:13-16 “Na mtu huyu akawa mkuu, akazidi kusitawi, hata akawa mkuu sana. Akawa na mali ya kondoo, na mali ya ng'ombe, na watumwa wengi. Hao Wafilisti wakamhusudu. Na vile visima vyote walivyochimba watumwa wa baba yake, siku za Ibrahimu babaye, Wafilisti walikuwa wamevifukia, wakavijaza kifusi. Abimeleki akamwambia Isaka, Utoke kwetu, maana wewe una nguvu sana kuliko sisi.”

 

·         Isaka alinyimwa nafasi – Mgogoro wa visima pamoja na kufukuzwa katika nchi ya Wafilisti wakati wote ilikuwa inalenga kumnyima Isaka ustawi, adui alikuwa anawekwa vikwazo ili kumnyima Isaka fursa ya utulivu na mafanikio, waligombea kisima cha kwanza akakiita Eseki maana yake UGOMVI, walifukia kisima cha pili na kukigombea akakiita Sitna maana yake UADUI kwa hiyo utaona Isaka anakabiliwa na ugomvi, uadui, upinzani, chuki na husuda, lakini kwa jinsi alivyokuwa muungwana na mwororo, hakugombana na mtu, tunajifunza ya kuwa tunaweza kushinda vita vingi kwa kuwa waungwana na kwa kutumia hekima kuliko kushindana na kujiingiza kwenye migogoro, kutokana na utulivu huu hatimaye Mungu aliamua kumpa utulivu halisi na hapa ndipo Bwana alipompa Nafasi, Rehoboth

 

Mwanzo 26:17-22 “Basi Isaka akatoka huko akapiga kambi katika bonde la Gerari, akakaa huko. Isaka akarudi akavichimbua vile visima vya maji walivyovichimba siku za Ibrahimu babaye; maana wale Wafilisti walikuwa wamevifukia baada ya kufa kwake Ibrahimu; naye akaviita majina kufuata majina alivyoviita babaye. Watumwa wa Isaka wakachimba katika lile bonde, wakapata kisima cha maji yanayobubujika. Wachungaji wa Gerari wakagombana na wachungaji wa Isaka wakisema, Maji haya ni yetu. Ndipo akakiita jina la kile kisima Eseki, kwa sababu waligombana naye. Wakachimba kisima kingine, wakagombania na hicho tena. Akakiita jina lake Sitna. Akaondoka huko akachimba kisima kingine, wala hicho hawakukigombania. Akakiita jina lake Rehobothi, akasema, Kwa kuwa sasa BWANA ametufanyia nafasi, nasi tutazidi katika nchi.”            

Kwa kuwa sasa Bwana ametufanyia nafasi

Mpenzi maisha ya Isaka  yanamkumbusha kila mmoja wetu kuwa changamoto unazozipitia ni za kawaida, kila mtu wa Mungu anaweza kupitia changamoto za iana mbalimbali katika maisha, Yesu alisema ulimwenguni mnayo dhiki, kwa sababu hiyo dhiki kama hizi ni za kawaida kwa watu wa Mungu, hata hivyo tunapoendelea kuwa na subira na kumtegemea Mungu hatimaye Mungu atatufanyia nafasi REHOBOTH Isaka kwa kweli hakuzitegemea akili zake mwenyewe, tunaweza kukiri kuwa kweli alikuwa na taaluma ya kuchimba visima lakini taaluma hiyo ingeweza kuigizwa na wengine au kusambazwa lakini hii ilikuwa ni ishara ya kuwa Mungu alikuwa pamoja naye, ukiri wake na kauli yake haikuwa kuwa sasa tumetoboa na badala yake alikiri kuwa ni Mungu ndiye aliyewafanyia  nafasi. Isaka aliendelea kubarikiwa mpaka adui zake walikuja kujipendekeza na kufanya Amani naye huku wakitambua kuwa hakika alikuwa na Mungu

Mwanzo 26:22-29 “Akaondoka huko akachimba kisima kingine, wala hicho hawakukigombania. Akakiita jina lake Rehobothi, akasema, Kwa kuwa sasa BWANA ametufanyia nafasi, nasi tutazidi katika nchi. Akapanda kutoka hapo mpaka Beer-sheba. BWANA akamtokea usiku uleule, akasema, Mimi ni Mungu wa Ibrahimu baba yako, usiogope, maana mimi ni pamoja nawe, nami nitakubarikia, na kuzidisha uzao wako kwa ajili ya Ibrahimu mtumishi wangu. Akajenga madhabahu huko, akaliitia jina la BWANA. Akapiga hema yake huko, na watumwa wa Isaka wakachimba kisima huko. Ndipo Abimeleki akamwendea kutoka Gerari, pamoja na Ahuzathi rafiki yake, na Fikoli, jemadari wa jeshi lake. Isaka akawauliza, Mbona mwanijia, nanyi mmenichukia, mkanifukuza kwenu?Wakasema, Hakika tuliona ya kwamba BWANA alikuwa pamoja nawe; nasi tukasema, Na tuapiane, sisi na wewe, na kufanya mapatano nawe ya kuwa hutatutenda mabaya, iwapo sisi hatukukugusa wewe, wala hatukukutendea ila mema, tukakuacha uende zako kwa amani; nawe sasa u mbarikiwa wa BWANA.”

Mambo ya kujifunza kutokana na maisha ya Isaka hapo:-

1.       Mungu ndiye anayetengeneza nafasi – Isaka hakusema kwamba tumetoboa, au tumewapiga bao Wafilisti au hawatuwezi hapana, yeye alisema sasa Bwana ametufanyia nafasi na tutazidi kuongezeka alisema haya kutokana na amani kwamba sasa maadui waliogopa kumfuatilia, dhamiri zao ziliwashitaki kwamba wataendelea na dhuluma zao mpaka lini mafanikio ya kweli ni yale ambayo Bwana ndiye anayekupigania, adui zako wanatamani usiwepo lakini wewe unaendelea kustawi na sababu ya ustawi wako inagunduliwa wazi kuwa ni Mungu, Mungu akikuandalia mazingira inapendeza sana kuliko wewe mwenyewe ukijilazimishia mazingira ya mafanikio

 

Zaburi 127:1 “Bwana asipoijenga nyumba Waijengao wafanya kazi bure. Bwana asipoulinda mji Yeye aulindaye akesha bure.”          

 

2.       Mafanikio ya kweli yanahitaji uvumilivu – wako watu ambao wanatamaa ya mafanikio na wanadhani kuwa mafanikio yanakuja kwa kuamka tu asubuhi, au kwa kuyalazimisha, nimeona watu wengi sana hasa vijana wanataka kila kitu kitokee kwa haraka lakini ni muhimu kuwa wavumilivu na kuwa wenye subira kwa sababu Mungu sio dhalimu kwa wakati wake atafanya, Isaka alivumilia, dhihaka, utasa, huzuni, njaa, wivu, ugomvi, kufukuzwa, uadui, dhuluma na kadhalika, alikuwa na nguvu kubwa sana lakini hakuitumia kupigana na adui zake  na kisha Bwana mwenyewe alimfanyia nafasi, hatupaswi kujipigania, hatupawi kukata tamaa hata kama Eseki na Sitna zitatokea katika maisha yetu hatimaye REHOBOTH italetwa na Bwana  kila mtu wa Mungu ajifunze ya kuwa anahitaji uvumilivu Saburi na mambo hayatakuja kuwa wakati mwingine kwa haraka kama tunavyofikiri

 

3.       Mungu anapokufungulia mlango Rehoboth - anakutengenezea mazingira ya kuongezeka, anakufanya ukue, huduma yako itakua, familia yako itaongezeka, uchumi wako utakuwa, Kiroho utakuwa, ushawishi utaiongezeka  utaogopwa, utaabudu kwa Amani na usalama, utafutwa machozi, adui zako watakuja kupatana na wewe wao wenyewe, utafurahia ndoa yako, utamfurahia Bwana Mungu wako, utafurahia biashara zako, utafurahia mifugo na kilimo, utaongeza maarifa hekima na elimu, utatimiza makusudi ya Mungu utakuwa na shuhuda, utatumika  

 

Zaburi 4:1-5 “Ee Mungu wa haki yangu, uniitikie niitapo; Umenifanyizia nafasi wakati wa shida; Unifadhili na kuisikia sala yangu. Enyi wanadamu, hata lini utukufu wangu utafedheheka? Je! Mtapenda ubatili na kutafuta uongo? Bali jueni ya kuwa Bwana amejiteulia mtauwa; Bwana atasikia nimwitapo. Mwe na hofu wala msitende dhambi, Tafakarini vitandani mwenu na kutulia. Toeni dhabihu za haki, Na kumtumaini Bwana

Ndugu zangu wapenzi kaka zangu na dada zangu, haijalishi ni maisha ya namna gani unayapitia, tambua tu kuwa dunia haina huruma hata kidogo na maisha yako, ni lazima umuwekee Mungu tumaini lako, unapojikita katika kumtegemea Mungu na kujiepusha na migogoro kisha wewe kuwa sababu ya Amani Mungu wa Ibrahimu, na wa Isaka na Yakobo baba zetu hatatuacha dunia yote na kila mtu anayesikia shuhuda zako atajua wazi kuwa Bwana yuko pamoja nawe, Bwana atakupigania nawe utanyamaza kimya, adui zako watakuja kukusujudia, hiki ndicho kilichomtokea Isaka Bwana alikuwa pamoja naye mpaka adui zake walilitambua hilo na kufanya Amani naye, wewe hupigani mwenyewe yuko anayekupigania naye yu hai katika jina la Yesu Kristo mwana wa Mungu aliye hai, Amen!

Na. Rev. Innocent Samuel Kamote.

Mkuu wa wajenzi mwenye Hekima.

Jumapili, 28 Juni 2026

Mwenende kama ulivyo wajibu wenu kwa Bwana!


Wakolosai 1:9-11 “Kwa sababu hiyo sisi nasi, tangu siku ile tuliposikia, hatuachi kufanya maombi na dua kwa ajili yenu, ili mjazwe maarifa ya mapenzi yake katika hekima yote na ufahamu wa rohoni; MWENENDE KAMA ULIVYO WAJIBU WENU KWA BWANA, mkimpendeza kabisa; mkizaa matunda kwa kila kazi njema, na kuzidi katika maarifa ya Mungu; mkiwezeshwa kwa uwezo wote, kwa kadiri ya nguvu ya utukufu wake, mpate kuwa na saburi ya kila namna na uvumilivu pamoja na furaha; mkimshukuru Baba, aliyewastahilisha kupokea sehemu ya urithi wa watakatifu katika nuru.”

 



Utangulizi:

Ni muhimu kufahamu kuwa mara baada ya kuwa tumeokolewa kwa neema ya Mungu, kwa njia ya imani, tunapaswa sana kuzingatia mwenendo wetu, Mtu aliyeokoka hataishi maisha anayojitakia tu kwa sababu ameokolewa, Lakini maandiko yanatoa maelekezo ya jinsi tunavyopaswa kuishi, yaani uko wajibu wetu tunaopaswa kutembea katika huo ili tuweze kuwa mfano wa kuigwa kama wana wa Mungu tuwapo hapa ulimwenguni, mwenendo huo ni wa lazima na wala sio wa hiyari, tunapaswa kuendenda kama vile Yesu Kristo mwenyewe alivyoenenda hapa duniani.

 

1Yohana 2:4-6 “Yeye asemaye, Nimemjua, wala hazishiki amri zake, ni mwongo, wala kweli haimo ndani yake. Lakini yeye alishikaye neno lake, katika huyo upendo wa Mungu umekamilika kweli kweli. Katika hili twajua ya kuwa tumo ndani yake. Yeye asemaye ya kuwa anakaa ndani yake, imempasa KUENENDA mwenyewe vile vile kama yeye ALIVYOENENDA.”

 

Katika maandiko yetu ya Msingi Paulo mtume anawaandikia Wakolosai aina ya maombi anayowaombea na kuwalekeza watu hao wajazwe maarifa ya mapenzi yake katika hekima yote na ufahamu wa rohoni ili kwamba waenende kama ulivyo wajibu wao kwa Bwana wakimpendeza yeye Kabisa!, Kumbe tunagundua ya kuwa kuna namna basi Wakristo tunapaswa kuenenda na swala hili liko wazi kabisa katika neno la Mungu. Kuna namna ya kutembea katika ulimwengu huu

 

Wafilipi 2:14-15 “Yatendeni mambo yote pasipo manung'uniko wala mashindano, mpate kuwa wana wa Mungu wasio na lawama, wala udanganyifu, wasio na ila kati ya kizazi chenye ukaidi, kilichopotoka; ambao kati ya hao mnaonekana kuwa kama mianga katika ulimwengu,”

 

Tito 2:11-12 “Maana neema ya Mungu iwaokoayo wanadamu wote imefunuliwa; nayo yatufundisha kukataa ubaya na tamaa za kidunia; tupate kuishi kwa kiasi, na haki, na utauwa, katika ulimwengu huu wa sasa;

 

Wakolosai 2:4-6 “Nasema neno hili, mtu asije akawadanganya kwa maneno ya kuwashawishi. Maana nijapokuwa sipo kwa mwili, lakini nipo pamoja nanyi kwa roho, nikifurahi na kuuona utaratibu wenu na uthabiti wa imani yenu katika Kristo. Basi kama mlivyompokea Kristo Yesu, Bwana, ENENDENI vivyo hivyo katika yeye;”

 

Kwa msingi huo utaweza kuona kuwa maandiko matakatifu yana namna ambayo kwamba Roho Mtakatifu ametukusudia sisi kuenenda sawasawa na maelekezo yanayotolewa katika maandiko lakini ili tuweze kuendelea kuelewa vizuri hatuna budi kufahamu maswala kadhaa ikiwa ni pamoja na maana ya neno mwenendo, tutajifunza somo hili Mwenende kama ulivyo wajibu wenu kwa Bwana! Kwa kuzingatia vipengele muhimu vitatu vifuatavyo;-

 

·         Maana ya neno mwenendo.

·         Jinsi inavyotupasa kuenenda.

·         Mwenende kama ulivyo wajibu wenu kwa Bwana!

 

Maana ya neno mwenendo.

 

Neno mwenendo ambalo limejitokeza zaidi ya mara 13 katika maandiko ya Kiyunani linasomeka kama “AnastrophÄ“” ambalo katika Biblia ya kiingereza linasomeka kama “conversation”, au “Behavior” au “Conducts” Katika Biblia ya Kiswahili limetumika neno mawazo, au mtazamo, tabia au mwenendo  kwa mfano kabla ya kuokoka mtu anaweza kuwa na tabia au mwenendo  ua mawazo yanayomuongoza kuwa na tabia hiyo, kwa hiyo mwenendo ni jumla ya mtazamo wa mtu na mazingira yanayopelekea awe na tabia hiyo aliyo nayo, Paulo mtume kabla ya kuokoka alikuwa na mtazamo kuwa Ukristo sio imani ya kweli na kwa sababu hiyo aliwatesa sana Wakristo na kanisa la kwanza kwa sababu mtazamo wake ulipelekea kuwa na mwenendo au tabia aliyokuwa nayo kabla ya kukutana na Bwana Yesu.

 

Wagalatia 1:13Maana mmesikia habari za MWENENDO wangu zamani katika dini ya Kiyahudi, kwamba naliliudhi kanisa la Mungu kupita kiasi, nikaliharibu. Nami naliendelea katika dini ya Kiyahudi kuliko wengi walio hirimu zangu katika kabila yangu, nikajitahidi sana katika kuyashika mapokeo ya baba zangu. Lakini Mungu, aliyenitenga tangu tumboni mwa mama yangu, akaniita kwa neema yake,”

 

Kwa hiyo mtu aliyeokoka anapaswa kuwa na mabadiliko ya mwenendo wake wa kwanza au ule wa zamani na anapaswa kuvaa mwenendo mpya unaotembea katika hali ya uchaji wa Mungu kwa kuzingatia kweli, haki na utakatifu, kwa sababu hiyo mtu aliyemwamini Bwana anatarajiwa awe na mwenendo tofauti na ule aliokuwa akiuendea zamani, haya ni mabadiliko yanayoanzia kwemye mtazamo, fundisho na kuonekana katika tabia na mtazamo mpya unaompa Mungu utukufu baada ya kumpokea Yesu kama Bwana na mwokozi wa maisha yetu!

 

Waefeso 4:20-24 “Bali ninyi, sivyo mlivyojifunza Kristo; ikiwa mlimsikia mkafundishwa katika yeye, kama kweli ilivyo katika Yesu, mvue kwa habari ya MWENENDO wa kwanza utu wa zamani, unaoharibika kwa kuzifuata tamaa zenye kudanganya; na mfanywe wapya katika roho ya nia zenu; mkavae utu mpya, ulioumbwa kwa namna ya Mungu katika haki na utakatifu wa kweli.”

 

Jinsi inavyotupasa kuenenda.

 

Tumejifunza sasa maana ya mwenendo na tumeona jinsi maandiko yanavyotuelezea kuwa uko mwenendo ambao tuliuendea zamani kabla ya kuokolewa na sasa baada ya kuwa tumeokolewa kuna aina ya mwenendo ambao tunapaswa kuuenenda na bila kufundishwa wakati mwingine inaweza kuwa ngumu kwetu kujua ni mwenendo gani tunapaswa kuufuata? Kwa hiyo yako mambo kadhaa ambayo Biblia inatuasa kuyafuata au kuyajifunza ili yaweze kuwa dira na njia ya kuujenga mwenendo wetu na huo ndio wajibu wetu ambao umesisitizwa katika maandiko ya msingi kwamba Mwenende kama ulivyo wajibu wenu kwa Bwana ni wajibu upi huo hapa yako mambo kadhaa ya kuyaangalia

 

1.       Ni wajibu wetu kuenenda kwa utakatifu – Utakatifu ni moja ya mwenendo ambao watu waliookoka wanapaswa kuwa nao, ni muhimu kuelewa kuwa ni vigumu kumuona Mungu bila ya kuwa na mwenendo wa utakatifu, utakatifu ni nini hasa? Biblia ya Kiyunani inatumia neno “Hagio” ambalo ni sawa na neno la Kiingereza “Pure morally” au “Blameless  maana yake kuendenda kwa uadilifu, au kutembea bila lawama, wakati wote katika maisha yetu isitokee tumelaumiwa kama watu wabaya au kwa kutenda mambo yasiyo ya uadilifu

 

1Petro 1:14-16. “Kama watoto wa kutii msijifananishe na tamaa zenu za kwanza za ujinga wenu; bali kama yeye aliyewaita alivyo mtakatifu, ninyi nanyi iweni watakatifu katika MWENENDO wenu wote; kwa maana imeandikwa, Mtakuwa watakatifu kwa kuwa mimi ni mtakatifu.”

 

2.       Ni wajibu wetu kuendenda kwa imani – watu wa Mungu wanapaswa kuenenda kwa Imani, pasipo imani haiwezekani kumpendeza Mungu, kwa hiyo yote tuyatendayo tunapaswa kuyafanya kwa imani, Mungu aliwaangamiza wana wa Israel wengi jangwani kwa sababu ya kutokuamini kwao, tukiendenda kwa imani ni rahisi kumpendeza Mungu, watu wa Mungu wanapaswa kuliamini neno la Mungu na kulitii kwa imani na sio kwa kutegemea yale tuyaonayo kwa macho ya kibinadamu au mazingira yanayokuzunguka

 

2Wakorintho 5:6-8 “Basi siku zote tuna moyo mkuu; tena twajua ya kuwa, wakati tuwapo hapa katika mwili, tunakaa mbali na Bwana. (Maana TWAENENDA kwa imani, si kwa kuona.) Lakini tuna moyo mkuu; nasi tunaona ni afadhali kutokuwamo katika mwili na kukaa pamoja na Bwana.”

 

3.       Ni wajibu wetu kuenenda kwa Upendo – Kuenenda kwa upendo ni mojawapo ya agizo la watu wa Mungu, kuishi kwa upendo, kutembea kwa upendo kujawa na upendo maisha yetu ni lazima yaonyeshe upendo wa kujitoa kama vile Kristo alivyojitoa kwetu na kwa ulimwengu ili kila amuaminiye aokolewe, chuki, husuda na wivu, magombano, visasi na majungu kamwe sio mwenendo wanaopaswa kuwa nao watu ambao Kristo amewafia Msalabani kwa kujitoa kuliko kukuu hata tulipokuwa wenye dhambi

 

Waefeso 5:1-2 “Hivyo mfuateni Mungu, kama watoto wanaopendwa; MKAENENDE katika upendo, kama Kristo naye alivyowapenda ninyi tena akajitoa kwa ajili yetu, sadaka na dhabihu kwa Mungu, kuwa harufu ya manukato.”

 

4.       Ni wajibu wetu kuenenda nuruni – Kuenenda nuruni kwa ufupi maana yake ni kutembea kwa kuweka kipaumbele maswala na maagizo ya Mungu, Mungu ni Nuru, Yesu Kristo mwenyewe pia alisema yeye ni Nuru ya ulimwengu, kwa sababu hiyo tunapoweka kipaumbele maswala Yote ambayo Yesu Kristo ametufundisha na kumfuata, maana yake tunaendenda Nuruni, kwenda kinyume na maagizo ya neno la Mungu ni kuenenda gizani

 

1Yohana 1:5-7 “Na hii ndiyo habari tuliyoisikia kwake, na kuihubiri kwenu, ya kwamba Mungu ni nuru, wala giza lo lote hamna ndani yake.Tukisema ya kwamba twashirikiana naye, tena tukienenda gizani, twasema uongo, wala hatuifanyi iliyo kweli; bali TUKIENENDA NURUNI, kama yeye alivyo katika nuru, twashirikiana sisi kwa sisi, na damu yake Yesu, Mwana wake, yatusafisha dhambi yote.”

 

5.       Ni wajibu wetu kuenenda katika upya wa maisha – kutembea katika upya wa maisha kunamaanisha ni lazima maisha yetu yabadilike tuwe na mwenendo mpya na sio ule wa zamani, kabala ya kuokolewa, hatupaswi tena kuitumikia dhambi ambayo tuliiendea zamani kabla ya kukutana na Yesu, sasa kwa kuwa tumekutana na Yesu hatuna budi kuenenda katika upya huu wa maisha na kutembea na Mungu, uongo, ulevi, tamaa mbaya, uchafu, kiburi, masengenyo, ubinafsi na kujihesabia haki pamoja na maovu ya kila namna hayapaswi kuonekana tena kwa mtu anayewajibika kuenenda katika upya wa maisha

 

Warumi 6:4-6 “Basi tulizikwa pamoja naye kwa njia ya ubatizo katika mauti yake, kusudi kama Kristo alivyofufuka katika wafu kwa njia ya utukufu wa Baba, vivyo hivyo na sisi TUENENDE KATIKA UPYA WA UZIMA. Kwa maana kama mlivyounganika naye katika mfano wa mauti yake, kadhalika mtaunganika kwa mfano wa kufufuka kwake; mkijua neno hili, ya kuwa utu wetu wa kale ulisulibishwa pamoja naye, ili mwili wa dhambi ubatilike, tusitumikie dhambi tena;”

 

6.       Ni wajibu wetu kuenenda kwa Roho – kuenenda kwa Roho maana yake ni nini? Ni maisha ambayo Roho Mtakatifu ndiye anayetawala, kila mtu aliyeokolewa ni muhimu na lazima atoe nafasi na kumruhusu Roho Mtakatifu kuyaongoza na kuyatawala maisha yake katika kila nyanja ya maisha na kumruhusu yeye kutusaidia kukomaa kiroho na kuzaa matunda ya Roho Mtakatifu katika maisha yetu, maisha yako unayaongoza wewe mwenyewe au unamuachia Roho akuongoze? Kuenenda kwa roho ni kumuachia yeye atuongoze maisha yetu.

 

Wagalatia 5:16-23 “Basi nasema, ENENDENI kwa Roho, wala hamtazitimiza kamwe tamaa za mwili. Kwa sababu mwili hutamani ukishindana na Roho, na Roho kushindana na mwili; kwa maana hizi zimepingana, hata hamwezi kufanya mnayotaka. Lakini mkiongozwa na Roho, hampo chini ya sheria. Basi matendo ya mwili ni dhahiri, ndiyo haya, uasherati, uchafu, ufisadi, ibada ya sanamu, uchawi, uadui, ugomvi, wivu, hasira, fitina, faraka, uzushi, husuda, ulevi, ulafi, na mambo yanayofanana na hayo, katika hayo nawaambia mapema, kama nilivyokwisha kuwaambia, ya kwamba watu watendao mambo ya jinsi hiyo hawataurithi ufalme wa Mungu. Lakini tunda la Roho ni upendo, furaha, amani, uvumilivu, utu wema, fadhili, uaminifu, upole, kiasi; juu ya mambo kama hayo hakuna sheria.”

 

7.       Ni wajibu wetu kuenenda kama unavyostahili wito wetu – Kila mtu aliyeokolewa kuna namna Mungu amemuita amtumikie katika mazingira mbalimbali na huo ndio wito wako, hapa wito haimaanishi ule wito wa kumtumikia Mungu pekee, wito maalumu, unaweza kuwa Mwalimu, Polisi, Daktrari, Mtoza ushuru, Mwanasiasa na kadhalika Mungu anataka uwe na mwenendo mwema katika kila aina ya wito ulioitiwa au kokote kule unakokuweko hata kama wewe ni fundi cherehani, iko miiko ya utumishi katika kile eneo la wito wa maisha basi huko enenda kama unavyoustahili wito wako, zaidi sana katika nyumba ya Mungu  huku tukitunza amani.

 

Waefeso 4:1-3 Kwa hiyo nawasihi, mimi niliye mfungwa katika Bwana, MWENENDE kama inavyoustahili wito wenu mlioitiwa; kwa unyenyekevu wote na upole, kwa uvumilivu, mkichukuliana katika upendo; na kujitahidi kuuhifadhi umoja wa Roho katika kifungo cha amani.”

 

8.       Ni wajibu wetu kuenenda kwa Hekima – Ni kama maandiko yanatuambaia wazi kuwa muda wetu duniani sio wa kwetu ni muda wa Mungu, Ni muda ambao tumepewa kwa kusudi la kumtumikia Mungu na kutimiza kusudi lake au mapenzi yake kwa hiyo Muda ni wa maana sana kwa watu waliookoka na haupaswi kupotezwa bure, watu wanaopoteza muda wanaitwa wasio na hekima au wajinga, ni lazima tujiangalie tunautumiaje Muda hasa sisi waafrika, tunaweza kutumia muda mwingi sana kupiga soga ua kusengenya muda ambao tungeweza kuutumia kwaajili ya Mungu, kwa kuyajua mapenzi yake na kuyafanya

 

Waefeso 5:15-17 “Basi angalieni sana jinsi MNAVYOENENDA; si kama watu wasio na hekima bali kama watu wenye hekima; mkiukomboa wakati kwa maana zamani hizi ni za uovu. Kwa sababu hiyo msiwe wajinga, bali mfahamu ni nini yaliyo mapenzi ya Bwana.”

 

9.       Ni wajibu wetu kuenenda vilevile kama tulivyompokea Kristo – Kuenenda vile vile kama tulivyompokea Kristo hakumaanishi ubaki vilevile baada ya kuokoka, lakini maana yake kila siku tunapaswa kuishi vile vile sawasawa na mafundisho tunayoyapokea kwa Bwana wetu Yesu Kristo kupitia Mwalimu wa Kweli Roho Mtakatifu, huku ni kuendelea kudumisha uhusiano wetu na Mungu kwa kutii na kujileta katika neema yake kukua katika upendo, unyenyekevu na hekima na kuhakikisha kuwa haturudi nyuma tangu tulipoanza uhusiano wetu na yeye.

 

Wakolosai 2:6-7 “Basi kama mlivyompokea Kristo Yesu, Bwana, ENENDENI vivyo hivyo katika yeye; wenye shina na wenye kujengwa katika yeye; mmefanywa imara kwa imani, kama mlivyofundishwa; mkizidi kutoa shukrani.

 

10.   Ni wajibu wetu kuenenda kwa kuikulia neema – Tumeokolewa kwa neema sisi kama wana wa Mungu ni wana wa neema kwa msingi huo hatuna budi kukua kwa kuikulia neema ya Mungu ni neema ya Mungu ndiyo inayotusaidia katika, kuukulia wokovu na kukomaa kiroho kwa hiyo hatuna budi kujitoa sisi wenyewe na kuenenda kwa kuikulia neema kwa kuendelea kutenda mema

 

Waefeso 2:8-10 “Kwa maana mmeokolewa kwa neema, kwa njia ya imani; ambayo hiyo haikutokana na nafsi zenu, ni kipawa cha Mungu; wala si kwa matendo, mtu awaye yote asije akajisifu. Maana tu kazi yake, tuliumbwa katika Kristo Yesu, tutende matendo mema, ambayo tokea awali Mungu aliyatengeneza ili TUENENDE NAYO.”

 

Mwenende kama ulivyo wajibu wenu kwa Bwana!

 

Wokovu ni Msaada wa Mungu kwetu, hata hivyo tabia na mwenendo ni wajibu wetu na ndio maana neno la Mungu linasema mwenende kama ulivyo wajibu wenu kwa Bwana, ni wajibu wetu kujitoa kwa Mungu na kukubali neema ya Mungu ituendeshe katika maisha haya kama watoto wake uili tuweze kuwa na mvuto hapa ulimwenguni, mwenendo wetu una nafasi kubwa mbili, kuimarisha uhusiano wetu wa ndani na Mungu, na pili kuwavutia wengine au kuwafundisha kivitendo jinsi Mungu alivyo mwadilifu, kuenenda kama ulivyo wajibu wetu kwa Bwana kumpa Mungu heshima inayoonyesha kuwa Mungu anabadilisha  maisha ya watu wake, tunaweza kuitangaza injili hata bila kusema neno kupitia tu mwenendo mwema, aina binadamu wote duniani wanajua kiwango cha uadilifu ambao watu wa Mungu wanapaswa kuenenda na ndio maana ukifanya mambo ya ajabu wanajua, kutokana na umuhimu wa jambo hili Paulo mtume aliwaombea sana wakolosai wajazwe maarifa, na hekima na ufahamu wa rohoni ili waenende kama ulivyo wajibu wao kwa Bwana wakimpendeza kabisa sio hivyo tu wakiwavutia watu wengine wasioamini waweze kuokolewa ili hayo yatimie hatuna budi kujitoa na kuhakikisha vile vile tunajileta wenyewe kanisani katika ibada za mafundisho ili tukutane na neno la Mungu litakalotupoa hekima na maarifa ili tujue nemna inavyotupasa kuenenda

 

Wakolosai 1:9-11 “Kwa sababu hiyo sisi nasi, tangu siku ile tuliposikia, hatuachi kufanya maombi na dua kwa ajili yenu, ili mjazwe maarifa ya mapenzi yake katika hekima yote na ufahamu wa rohoni; MWENENDE KAMA ULIVYO WAJIBU WENU KWA BWANA, mkimpendeza kabisa; mkizaa matunda kwa kila kazi njema, na kuzidi katika maarifa ya Mungu; mkiwezeshwa kwa uwezo wote, kwa kadiri ya nguvu ya utukufu wake, mpate kuwa na saburi ya kila namna na uvumilivu pamoja na furaha; mkimshukuru Baba, aliyewastahilisha kupokea sehemu ya urithi wa watakatifu katika nuru.”

 

1Petro 3:1-2 “Kadhalika ninyi wake, watiini waume zenu; kusudi, ikiwa wako wasioliamini Neno, wavutwe kwa MWENENDO wa wake zao, pasipo lile Neno; wakiutazama MWENENDO wenu safi, na wa hofu.”

 

Mwenendo ni msingi muhimu sana katika maisha ya Ukristo, ni lazima kila Mkristo awe na mwenendo unaomuakisi Yesu Kristo na hii ni kanuni Muhimu sana katika maisha ya ukristo na mwenendo wa kibiblia, mwenendo mwema mbele ya watu wasiomjua Mungu huwavutia watu wengine wapate kuokolewa, na sio hivyo tu ni mwenendo ndio unaotusaidia kupata viongozi wa kanisa ambao mfano wao unaweza kuigizwa na wengine mwenendo unatajwa kama hekima na tabia nzuri, unatajwa kama utetezi tunaposingiziwa, unaonyesha kielelelzo kama viongozi katika nyumba ya Mungu kwa hivyo tukiwajibika vizuri kwa Bwana tutawavutia watu kukubali ukweli ya kuwa Mungu anaokoa na anabadilisha watu wake kwa sababu watu wataona mabadiliko makubwa ya mwenendo wetu.

 

Yakobo 3:11-13. “Je! Chemchemi katika jicho moja hutoa maji matamu na maji machungu? Ndugu zangu, Je! Mtini waweza kuzaa zeituni, au mzabibu kuzaa tini? Kadhalika chemchemi haiwezi kutoa maji ya chumvi na maji matamu. N'nani aliye na hekima na ufahamu kwenu? Na aonyeshe kazi zake kwa MWENENDO wake mzuri, katika upole wa hekima.”

 

1Timotheo 4:12 “Mtu awaye yote asiudharau ujana wako, bali uwe kielelezo kwao waaminio, katika usemi na MWENENDO, na katika upendo na imani na usafi.”

 

1Petro 2:12 “Mwe na MWENENDO mzuri kati ya Mataifa, ili, iwapo huwasingizia kuwa watenda mabaya, wayatazamapo matendo yenu mazuri, wamtukuze Mungu siku ya kujiliwa.”

 

Na Rev. Innocent Samuel Kamote

 

Mkuu wa wajenzi mwenye Hekima

Jumapili, 21 Juni 2026

Kumbe ni Lea badala ya Raheli!


Mwanzo 29:20-26 “Yakobo akatumika miaka saba kwa kumpata Raheli. Ikawa machoni pake kama siku chache tu kwa vile alivyompenda. Yakobo akamwambia Labani, Nipe mke wangu, maana siku zangu zimetimia; niingie kwake. Labani akakusanya watu wote wa mahali pale, akafanya karamu. Ikawa wakati wa jioni akamtwaa Lea, binti yake, akamletea Yakobo, naye akaingia kwake. Labani akampa Lea mjakazi wake Zilpa, awe mjakazi wake. Ikawa, kulipokuwa asubuhi, kumbe! Ni Lea. Akamwambia Labani, Nini hii uliyonitenda? Sikukutumikia kwa Raheli? Mbona umenidanganya? Labani akasema, Havitendeki hivi kwetu, kumtoa mdogo kabla ya mkubwa;”



Utangulizi:

Hakuna linalotokea kwa bahati mbaya Duniani, wakati mwingine Mungu anaweza kuruhusu, ufanye kazi, au biashara, au huduma au usomee fani ambayo kimsingi inaweza ikawa sio chaguo lako, na hali kadhalika unaweza kuwa katika mahusiano na mtu ambaye moyo wako unaweza usiwe umemridhia moja kwa moja isipokuwa ni kwa sababu ya mazingira fulani, katika maisha yangu nimekuwa karibu na wanafunzi na walimu na watu wa kada mbalimbali za kitaaluma, na nimesikia kwa masikio yangu wengine wakisema nilitaka kuchukua masomo ya Sayansi, lakini walimu walinishauri nichukue masomo ya Sanaa, nilitaka kuchukua masomo ya Sanaa lakini wazazi wangu walinishauri nichukue Sayansi, nilitaka kuwa daktari lakini serikali ilinipangia ualimu, nilitaka kuwa mwanasheria lakini nililazimika kuwa mwanahabari, nilikuwa na mipango yangu kadhaa lakini nimejikuta nimekuwa Mwalimu, Mungu katika hekima yake wakati mwingine anaweza kuruhusu ubebe mzigo ambao moyo wako hungependelea kuubeba kwa kusudi la kutimiza mpango wake usioweza kuuona kwa wakati huo au kwa macho yako na sio hivyo tu wakati mwingine Mungu anaruhusu hivyo kwaajili ya ukuaji wa kiroho, kukufundisha kuacha mapenzi yako na kusikiliza ya kwake, kukufundisha uvumilivu, kupenda kisichoweza kupendeka na kukunyima kutimiza mapenzi yako uli uweze kujisalimisha kwenye mapenzi yake, hali kama hiyo ndiyo iliyomtokea Yakobo wakati anataka kuoa, alijiandaa na kufanya kazi kwa bidii kwaajili ya Raheli lakini akaozwa Lea bila kutaka!, Kumbe ni Lea badala ya Raheli.

Mwanzo 29:16-20 “Labani alikuwa na binti wawili, jina la mkubwa ni Lea, na jina la mdogo ni Raheli. Naye Lea macho yake yalikuwa dhaifu, lakini Raheli alikuwa mzuri wa umbo, na mzuri uso. Yakobo akampenda Raheli akasema, Nitakutumikia miaka saba kwa kumpata Raheli, binti yako mdogo. Labani akasema, Afadhali nikupe wewe kuliko mtu mwingine; kaa kwangu. Yakobo akatumika miaka saba kwa kumpata Raheli. Ikawa machoni pake kama siku chache tu kwa vile alivyompenda.”

Kuna maumivu kiasi fulani ambayo wengine wanaweza wasiyaseme kwa maneno lakini yakaishia moyoni, maumivu ya kupata ua kufanya jambo ambalo kimsingi hujalipenda toka moyoni, hujalitamani, hujalitaka wala hujaliomba, au hujalisomea, unaweza kabisa katika maisha ukasomea ujuzi fulani kisha ukapangiwa mwingine, unaweza kuomba kazi fulani na ukapewa nyingine unaweza kutarajia kuwa ungeoa mke wa aina fulani au ukaolewa na mume wa aina fulani, lakini ukaishia kuolewa na mwingine, ungetaka idadi fulani ya watoto au watoto wa jinsia fulan unashangaa umepewa wa aina fulanii, au ulikuwa na ndoto ya maisha fulani na ukajikuta unaishi maisha tofauti, haya ndiyo yaliyo mtokea Yakobo, alipoenda kwa mjomba wake kuoa alikuwa na nia ya kumpata Raheli na kimsingi alimpenda Raheli aliwekeza nguvu zake na akili zake na hisia zake kwa Raheli, na akatumika miaka saba ili ampate kipenzi wake Raheli lakini siku ya harusi yake anaamka asubuhi kumbe ni Lea! Hali hii inawakuta watu wengi,  katika maisha kujikuta kuwa wana kile walichokua hawajakitaka, ujumbe huu ni kwa watu wanaopitia hali kama hiyo na Mungu ana makusudi na wewe na anataka kusema nawe, tutajifunza ujumbe huu KUMBE NI LEA BADALA YA RAHELI kwa kuzingatia vipengele muhimu vitatu  vifuatavyo:-

·         Inapokuwa Lea badala ya Raheli

·         Kumbe ni Lea badala ya Raheli

·         Kusudi la Mungu kupitia Lea

Inapokuwa Lea badala ya Raheli

Wote tutakuwa tunakumbuka kuwa baada ya Yakobo kuchukua mbaraka wa Esau na mgogoro kujitokeza katika familia Rebeka alimshauri Isaka kuwa kijana wao na aende kwa kaka yake Rebeka yaani Labani ili ajipatie mke huko badala ya kujitwalia mke katikati ya Wakanaani ambao roho yake Rebeka haikuwaridhia, Yakobo alisafiri kuelekea Haran kwa mjomba wake Labani ili ajipatie mke huko na alipofika huko kimsingi Yakobo alimpenda sana Raheli kwa sababu ndiye aliyekuwa anamvutia kimwili na kiumbo na kwa uzuri, walipatana na mjomba wake kuwa mahari itakuwa ni kumtumikia kwa miaka 7 kwaajili ya Raheli, kwa hiyo Yakobo alifanya kazi kwa bidii sana kwaajili ya kile alichokuwa amekiona, amekitamani na kukipenda, mke wa ndoto yake, stori nzima iko hapa:-

Mwanzo 29:16-30 “Labani alikuwa na binti wawili, jina la mkubwa ni Lea, na jina la mdogo ni Raheli. Naye Lea macho yake yalikuwa dhaifu, lakini Raheli alikuwa mzuri wa umbo, na mzuri uso. Yakobo akampenda Raheli akasema, Nitakutumikia miaka saba kwa kumpata Raheli, binti yako mdogo. Labani akasema, Afadhali nikupe wewe kuliko mtu mwingine; kaa kwangu.Yakobo akatumika miaka saba kwa kumpata Raheli. Ikawa machoni pake kama siku chache tu kwa vile alivyompenda. Yakobo akamwambia Labani, Nipe mke wangu, maana siku zangu zimetimia; niingie kwake. Labani akakusanya watu wote wa mahali pale, akafanya karamu.Ikawa wakati wa jioni akamtwaa Lea, binti yake, akamletea Yakobo, naye akaingia kwake. Labani akampa Lea mjakazi wake Zilpa, awe mjakazi wake. Ikawa, kulipokuwa asubuhi, kumbe! Ni Lea. Akamwambia Labani, Nini hii uliyonitenda? Sikukutumikia kwa Raheli? Mbona umenidanganya? Labani akasema, Havitendeki hivi kwetu, kumtoa mdogo kabla ya mkubwa; timiza siku zake saba, nasi tutakupa huyu naye kwa utumishi utakaonitumikia, miaka saba mingine. Yakobo akafanya hivi, akatimiza siku zake saba. Naye akampa Raheli binti yake kuwa mkewe. Labani akampa binti yake Raheli mjakazi wake Bilha, awe mjakazi wake. Akaingia kwa Raheli naye, akampenda Raheli kuliko Lea, akatumika kwa ajili yake miaka saba mingine.”

Unaweza kuona mtu anafanya kazi kwa bidii na kwa kujituma kweli kweli akiwa na ndoto ya kumpata Raheli lakini hatimaye anakuja kupewa Lea, hili linaweza kuwa jambo lenye kuumiza sana kwamba unafanya kazi, unasoma au unajituma kwaajili ya malengo fulani alafu unakuja kujikuta ni kama ulimwengu unataka ufanye jambo lingine, jambo hili linaumiza, unatoa juhudi zako zote, unatoa muda wako wote, unawekeza moyo wako wote lakini matokeo yanakuwa sio yale uliyoyatarajia, hali hii iko hivyo duniani, kuna watu wamewapenda sana wachumba zao, wakawafulia, wakawapikia, wakawa wakiwajulia hali lakini na kuwapa kila kitu, lakini yule bwana akaja akaoa mwanamke mwingine, kuna watu wamejitoa kwaajili ya wachumba wao wakawasomesha wakawahudumia na kuwafadhili, hata wakafunga na kuomba kwaajili yao kwa kulia, lakini wakaja kuolewa na mwanaume mwingine, kuna watu walikuwa na ndoto ya kuendesha ndege lakini leo ni Askari polisi, kuna watu walitaka kuwa madaktari lakini leo ni walimu, Moyo wako unaweza kuchoka na kuumia na kuumizwa na matarajio yaliyovunjika na unaweza kujiuliza Mungu kwa nini hali hii inakuwa hivi? Unasomea fani Fulani kisha unakuja kupata kazi flani tofauti na ile uliyoisomea na iliyoko moyoni mwako! Wala sicho ulichokitarajia, unahisi kuchanganyikiwa, unahisi kuumia na unaanza kumuhoji Mungu! Imekuwaje? Ndoto yangu ilikuwa hii mbona nafanya jambo hili?

Mithali 13:12 “Kilichotarajiwa kikikawia kuja, moyo huugua. Bali haja ya mtu ikipatikana, ni mti wa uzima.”

Tunao watu wengi sana leo hii katika jamii ambao mioyo yao imejeruhiwa kwa kuwa na matokeo wasiyoyatarajia, mtu amesoma kwa bidii na kufanya mtihani wake kwa umakini anakuja kupata Division three ambayo hakuitegemea, unaweza kuolewa na mume ambaye  hata hukuwa na hata hisia naye, unaweza kuwa na mke ambaye huna hata hisia naye lakini mnajikuta ndio mnaishi, yako maisha ambayo unaweza kuwa ndani yake lakini moyo wako ukawa haupo humo, haki hii ndiyo ilityomtokea Yakobo anampenda Raheli na ameganya kqzi miaka saba kwaajili yake, lakini amepewa Lea, kwa hiyo katika maisha yetu inapokuwa Lea badala ya Raheli watu hukosa amani na furaha na kuona kama maisha yameshakataa na wakati mwingine unaweza kuwaza na kufikiri umekosea wapi katika kaninu za maisha, unaweza kujikuta hufurahii maisha, hufurahii kazi, unakosa furaha kwa kile ulichonacho na ukijilinganisha na wengine ndio unachoka unaweza kudhani wewe una balaa, lakini nataka nikugusie kuwa Mungu ana mpango!, Hakuna jambo lolote linalotokeaau kukupata nje ya mpango wa Mungu, hapa duniani hatujaja kutimiza mpango wetu, tumekuja duniani kutimiza mpango na mapenzi ya Mungu, hivyo sio jambo la ajabu yakakupata yaliyo mageni

Kumbe ni Lea badala ya Raheli

Neno la Mungu linaonyesha ya kuwa njia za Mungu ziko juu sana kuliko njia za mwanadamu na wala mawazo yetu si kama mawazo yake, njia za Mungu ziko juu sana, mpango wa Mungu ni mkuu kuliko matakwa ya mwanadamu, Mungu hafanyi kazi kwa kusikiliza hisia zeu, ana mpango mkubwa sana kuliko hisia zako, Hapa duniani ulizaliwa kwa kusudi la Mungu na kwa sababu hiyo mwenye mji wake ni Mungu na mwenye mpango wake ni yeye kwa hiyo wewe unaweza kumtaka Raheli lakini Mungu akakupa Lea, unaweza kudhani kuwa dunia imekulazimisha Lea na we ulitaka Raheli lakini, Lea ndio mpango kamili wa Mungu. Raheli unaweza kuwa sio mpango wa kudumu wala wa milele lakini Lea unaweza kuwa mpango wa Mungu wa kudumu na wa milele, na wenye faida unajua nini  watoto wote maalumu ambao Mungu alikuwa na kusudi lake la kudumu walipita kwa Lea na sio Raheli

Mwanzo 29:31-35 “BWANA akaona ya kwamba Lea hakupendwa, naye akafungua tumbo lake; bali Raheli alikuwa hazai. Lea akapata mimba akazaa mwana, akampa jina lake, Reubeni, maana alisema, Kwa kuwa BWANA ameona teso langu; sasa mume wangu atanipenda. Akapata mimba tena akazaa mwana, akasema, Kwa kuwa BWANA amesikia ya kwamba mimi sikupendwa, amenipa na huyu; akamwita jina lake Simeoni. Akapata mimba tena, akazaa mwana, akasema, Basi wakati huu mume wangu ataungana nami, kwa sababu nimemzalia wana watatu. Kwa hiyo akamwita jina lake Lawi. Akapata mimba tena, akazaa mwana. Akasema, Mara hii nitamsifu BWANA; kwa hiyo akamwita jina lake Yuda; akaacha kuzaa.”

Mungu aliwatumia Walawi, kutoka kwa Lea kuwa makuhani kwaajili ya utumishi wa Mungu katika nyumba yake na Mungu na Mungu alimtumia Yuda kutoka kwa Lea kuleta viongozi mashuhuri na wacha Mungu kama Daudi na kupitia Lea na Yuda alimleta Yesu Kristo

Mathayo 1:1-2.“Kitabu cha ukoo wa Yesu Kristo, mwana wa Daudi, mwana wa Ibrahimu. Ibrahimu alimzaa Isaka; Isaka akamzaa Yakobo; Yakobo akamzaa Yuda na ndugu zake;”

Mungu aliruhusu Lea kuwepo katika maisha ya Yakobo kwa sababu Lea ndio ulikuwa mpango wa Mungu, Lea alikuwa ni darasa la unyenyekevu, Lea alikuwa ni chuo cha uvumilivu, Lea alikuwa ni shule ya haki ya Mungu, Lea ilikuwa ni shule ya kujifunza kupenda kile ambacho Mungu amekupangia, Mungu anatufundisha kumfuata yeye na sio hisia zetu, Lazima ufike wakati katika maisha yetu tuamue kufuata hisia zetu au kutimiza mpango wa Mungu, Lea alilazimika kutaka kumpendeza Yakobo lakini hata pamoja na kumzalia watoto wengi wa kume mfuluzizo bado Yakobo hakuona nguvu za Mungu, Lea aliamua kumuita mtoto wake Yuda akisema NITAMSIFU BWANA Furaha ya kweli haipatikani kwa wanadamu bali inapatikana kwa Mungu, Mungu aliona kitu ndani ya Lea ambacho kimsingi hakikuweko ndani ya Raheli Mungu anaona kile ambacho wanadamu hawakioni, Lea hakuwa mzuri wa uso lakini alikuwa mzuri moyoni, Yule aliyeyependwa na aliyekuwa mzuri wa uso moyoni hakuwa ameshikamana na Mungu na aliibeba  kwa kuiiba miungu ya baba yake na alikufa baaadae kwa neno la Yakobo ona:-

Mwanzo 31:19-35 “Basi Labani alikuwa amekwenda kuwakata manyoya kondoo zake, na Raheli akaviiba vinyago vya babaye. Yakobo akamhadaa Labani, Mshami, kwa kuwa hakumwambia ya kwamba anakimbia. Basi akakimbia yeye na yote aliyokuwa nayo; akaondoka akauvuka mto, akaelekeza uso wake kwenda mlima wa Gileadi. Hata siku ya tatu Labani akaambiwa ya kwamba Yakobo amekimbia, akatwaa ndugu zake pamoja naye, akamfuata mwendo wa siku saba. Akampata katika mlima wa Gileadi. Mungu akamjia Labani, Mshami, katika ndoto ya usiku, akamwambia, Ujihadhari, usimwambie Yakobo neno la heri wala la shari. Labani akamfikia Yakobo, na Yakobo alikuwa amepiga hema zake katika mlima, na Labani na ndugu zake wakapiga hema zao katika mlima wa Gileadi. Labani akamwambia Yakobo, Umefanya nini? Umenihadaa, ukawachukua binti zangu kama mateka waliotwaliwa kwa upanga. Mbona umekimbia kwa siri ukanihadaa, wala hukuniambia, nipate kuagana nawe uende zako kwa furaha, na nyimbo, na ngoma, na kinubi? Wala hukuniacha niwabusu wanangu, na binti zangu; basi umetenda upumbavu. Ninao uwezo mkononi mwangu wa kukufanyia madhara; lakini Mungu wa baba yako usiku huu ameniambia, akisema, Ujihadhari, usimwambie Yakobo neno la heri wala la shari. Basi sasa, umetoka kwa sababu umetamani sana nyumba ya baba yako. Mbona basi umeiiba miungu yangu? Yakobo akajibu, akamwambia Labani, Kwa sababu naliogopa, nikasema, Usije ukaninyang'anya binti zako kwa nguvu. Awaye yote utakayemwona kuwa nayo miungu yako, yeye asiishi. Mbele ya ndugu zetu ukitambue kilicho chako kwangu, ukakichukue. Maana Yakobo hakujua ya kwamba Raheli ameiiba. Labani akaingia katika hema ya Yakobo, na hema ya Lea, na hema ya vijakazi wawili, wala hakuiona. Akatoka katika hema ya Lea, akaingia katika hema ya Raheli. Basi Raheli alikuwa amevitwaa vile vinyago ameviweka katika matandiko ya ngamia, na kuvikalia. Labani akapapasa hema yote wala hakuviona. Naye Raheli akamwambia babaye, Bwana wangu asikasirike kwa sababu siwezi kuinuka mbele yako, maana nimeshikwa na mambo ya kike. Akatafuta, wala hakuviona vile vinyago.”

Raheli alikuwa muabudu miungu, aliiba miungu ya baba yake Neno vinyago linalotajwa hapo katika Kiebrania linatajwa kama “Teraphim” ambao ni miungu midogo midogo yenye sura kama ya mwanadamu ambayo ilichongwa na kuabudiwa zamani hasa huko mashariki ya mbali na ambayo ilitumika kwa uganga na uchawi na kupigia ramli, miungu hii ilichongwa kwa mfano wa wanadamu na iliyorithiwa toka mababu na mababu na ilirithishwa kwa viongozi wa familia kwa hiyo kuwa na miungu hiyo kulimaanisha kutaka kuwa kiongozi wa familia  na Labani alipokuja kuulizia miungu hiyo Raheli aliificha, Yakobo bila kuelewa alimwambia  Labani yeye atakayekutwa na miungu yako na asiishi, tukio hili lilipelekea kifo cha mapema cha Raheli, Kumbe Lea alimuabudu Mungu wa kweli lakini Raheli miungu!

Mwanzo 35:16-18 “Wakasafiri kutoka Betheli, hata ukabaki mwendo wa kitambo tu kufika Efrathi, Raheli akashikwa na utungu wa kuzaa, na utungu wake ulikuwa mzito. Ikawa alipokuwa anashikwa sana na utungu, mzalisha akamwambia, Usiogope, maana sasa utamzaa mwanamume mwingine. Ikawa hapo katika kutoa roho yake, maana alikufa, akamwita jina lake Benoni, lakini babaye alimwita Benyamini.”

Je bado una huzuni ya kumkosa Raheli? Mungu alikuwa na mpango, sio kila Raheli ni Baraka na sio kila Lea ni Laana wakati mwingine Raheli ni tamaa yako na Lea ni mapenzi ya Mungu kwako, Mpango wa Mungu haujafichwa ndani ya kile unachikipenda bali uko ndani ya kile alichokupa, acha kutokukubaliana na Lea katika maisha yako, Lea sasa anahitaji upendo wako, ni muhimu sasa ukakubaliana na kile ambacho Mungu amekiruhusu katika maisha yako, ni lazima ukubali mapenzi ya Mungu na kutafuta kusudi la ndani la hali uliyo nayo, badala ya kujutia kile ulichonyimwa furahia kile ulichopewa na Mungu na kipokee kwa shukurani maana katika hilo uko mpango wa Mungu, Yesu anatoka kwa Lea na sio kwa Raheli, kile usichokipenda kinaweza kubeba hatima yako! Na kusudi la Mungu katika mpango wake, yako mambo tunaweza kuchagua na yako mambo Mungu mwenyewe anakuchagulia, furahia kile Mungu amekuchagulia, hakuna bahati mbaya katika kile Mungu amekupangia, oooo kumbe ni Lea badala ya Raheli.

Kusudi la Mungu kupitia Lea

Mungu anataka kutufunza hapa kuwa wakati mwingine katika hekima yake atafanya mambo kinyume na yale tunayoyatarajia ambayo kimsingi ni shauku na tamaa zetu au hisia zetu, Mungu anataka kuivunja ile hali ya kujitegemea katika maamuzi yetu anataka ukomavu anataka kurekebisha tabia zetu anataka kutuumbia moyo wa kuwa na uhusiano wa karibu sana na yeye ili tumtegemee yeye, hali hizo zote zinaruhusiwa kwaajili ya ukamilifu wetu kwa hiyo wale wote ambao wako katika hali kama ile aliyoipitia Yakobo wanapaswa kuelewa kuwa ni mchakao wa Mungu utimize mapenzi yake na sio ya kwako kwa hiyo fanya kwa upendo na uaminifu kile ambacho Mungu amekuchagulia.

Warumi 8:28-29 “Nasi twajua ya kuwa katika mambo yote Mungu hufanya kazi pamoja na wale wampendao katika kuwapatia mema, yaani, wale walioitwa kwa kusudi lake. Maana wale aliowajua tangu asili, aliwachagua tangu asili wafananishwe na mfano wa Mwana wake, ili yeye awe mzaliwa wa kwanza miongoni mwa ndugu wengi.”

Mungu anataka tuache kujitegemea na kujitumainia na badala yake tuishi kwa kumtegemea yeye, Mungu ataupiga chini mpango wetu wa ubinafsi na atabadilisha mambo ili tumtegemee yeye

2Wakorintho 12:7-9. “Na makusudi nisipate kujivuna kupita kiasi, kwa wingi wa mafunuo hayo nalipewa mwiba katika mwili, mjumbe wa Shetani ili anipige, nisije nikajivuna kupita kiasi. Kwa ajili ya kitu hicho nalimsihi Bwana mara tatu kwamba kinitoke.Naye akaniambia, Neema yangu yakutosha; maana uweza wangu hutimilika katika udhaifu. Basi nitajisifia udhaifu wangu kwa furaha nyingi, ili uweza wa Kristo ukae juu yangu.”

Mungu anataka utii hata katika mazingira magumu, kwa msingi huo badala ya kujiuliza kwanini mimi ninayapitia haya wewe jiulize Mungu atatukuzwaje kwenye jambo hili, Je kwa kuwa tumepewa uhuru wa kuchagua wadhani ya kuwa Mungu hana nafasi ya kuonyesha ubwana wake katika maisha yetu? Ubinafsi wetu na starehe zetu lazima zife linapokuja swala la kutimiza mpango wa Mungu, Kumbe ni Lea badala ya Raheli.

Na. Rev. Innocent Samuel Kamote

Mkuu wa wajenzi mwenye Hekima