Isaya 42:1-4 “Tazama mtumishi wangu
nimtegemezaye; mteule wangu, ambaye nafsi yangu imependezwa naye; nimetia roho
yangu juu yake; naye atawatolea mataifa hukumu. Hatalia, wala hatapaza sauti
yake, wala kuifanya isikiwe katika njia kuu. Mwanzi uliopondeka hatauvunja,
wala utambi utokao moshi hatauzima; atatokeza hukumu kwa kweli. Hatazimia, wala
hatakata tamaa, hata atakapoweka hukumu duniani; na visiwa vitaingojea sheria
yake.”
Utangulizi:
Kaka zangu na dada zangu katika
Bwana, Leo tutachukua muda kujifunza mojawapo ya unabii wa muhimu sana katika
huduma ya Masihi ambao kimsingi ulikuja kutimizwa katika agano jipya, Wakati wa
huduma ya Masihi hapa duniani, Unabii huu ambao kimsingi unatufundisha kusudi
kubwa la huduma na moyo wa Masihi Yesu Kristo hapa ulimwenguni, jinsi
alivyojawa na huduma iliyojaa rehema na upendo unaopitiliza mipaka ya kawaida
ya huduma za kibinadamu na kidini.
Mathayo 12:15-21 “Naye Yesu hali
akiyafahamu hayo akaondoka huko; na watu wengi wakamfuata; akawaponya wote,
akawakataza wasimdhihirishe; ili litimie neno lililonenwa na nabii Isaya,
akisema, Tazama, mtumishi wangu niliyemteua; Mpendwa wangu, moyo wangu
uliyependezwa naye; Nitatia roho yangu juu yake, Naye atawatangazia Mataifa
hukumu. Hatateta wala hatapaza sauti yake; Wala mtu hatasikia sauti yake njiani.
Mwanzi uliopondeka hatauvunja, Wala utambi utokao moshi hatauzima, Hata
ailetapo hukumu ikashinda. Na jina lake Mataifa watalitumainia.”
Kwa ujumla unabii wa Isaya na
kutimia kwake kunatukumbusha jambo muhimu sana na lenye kutia moyo ya kuwa
Ufalme wa Mungu unatenda kazi katika msingi wa rehema, urejesho na huruma
zisizotikisika! “Mwanzi uliopondeka hatauvunja
na utambi utokao moshi hatauzima” vinawakilisha nini hasa katika ujumbe
huu? Bila shaka Mungu Roho Mtakatifu atatupa kuelewa; Tutajifunza somo hili
Mwanzi uliopondeka hatauvunja kwa kuzingatia vipengele vikuu vitatu
vifuatavyo:-
·
Ufahamu kuhusu mwanzi uliopondeka na utambi
utokao moshi
·
Huduma ya kimasihi mwanzi uliopondeka na utambi
utokao moshi
·
Mwanzi uliopondeka na utambi utokao moshi
Ufahamu kuhusu mwanzi uliopondeka na utambi utokao moshi.
Ni muhimu kufahamu kuwa usemi wa
“mwanzi uliopondeka na utambi utoka
moshi” ni usemi wenye maana gani kinabii kabla ya kuunganisha na kuangalia huduma
ya kimasihi itakavyokuwa, Neno mwanzi linalotumika katika maandiko ya
kiingereza linatumika neno “REEDS” ambalo
kwa Kiswahili maana yake ni nyasi, Hata hivyo nyasi ziko za aina mbalimbali,
kwa hiyo nyasi hizi katika
lugha ya Kiebrania zinaitwa kwa
kutumia neno Kāneh
kwa lugha ya Kilatini na Kiyunani linatumika neno Canna kwa kiingereza
Cane mmea huu kwa kawaida ulistawi
sana pembeni mwa mto Jordan katika
taifa la Israel kwa Kiswahili unaitwa
MWANZI, majani ya Mwanzi au Cane kwa
Kiyunani yanajulikana kama kálamos au Calamus, kwa Kiswahili
Kalamu. Nyakati za agano la kale kabla ya kuwepo kwa teknolojia ya uandishi
tuliyo nayo sasa Manabii na waandishi walitumia majani ya muanzi kama kalamu ya
kuandikia, waliyatumia majani haya na kuchovya kwenye wino na kuyatumia
kuandikia katika karatasi maalumu za nyakati hizo (Papyrus) au Magombo ya
chuo ya ngozi, walichovya katika
bakuli la wino kwa kutumia majani hayo yaliyoitwa kalamu na kisha kuyatumia kuandikia endapo kalamu ingechoka au
kupondeka waliitupa na kuchomoa jani lingine la muanzi yaani kalamu na kutoka
kwenye kitita cha majani hayo na kulitumia kuandika, waandishi wangeifanya kazi
hiyo ngumu kutwa nzima na usiku, huku usiku wakitumia taa ya kibatali
iliyotumia mafuta na utambi, manabii na waandishi walifanya kazi ya kuandika
mpaka mafuta yangewaishia na taa ikazimika na utambi ungebaki unafuka moshi
hapo wangezima kabisa na kulala wakiwa wamechoka sana kitendo cha kuvunjika kwa
Kalamu au kuisha kwa utambi kulikwamisha kwa kiwango kikubwa kazi nzima ya
uandishi, wakati huu nabii Isaya alipokea ujumbe wa kinabii kwamba kazi hiyo ya
kuchosha itakuwa nyepesi, wakati wa Masihi, na wakati wa Masihi kalamu
haitavunjika wala utambi hautaisha na kufuka moshi, uwepo wake utasababisha
uzima katika mazingira yote.
Isaya 42:1-3 “Tazama mtumishi wangu
nimtegemezaye; mteule wangu, ambaye nafsi yangu imependezwa naye; nimetia roho
yangu juu yake; naye atawatolea mataifa hukumu. Hatalia, wala hatapaza sauti
yake, wala kuifanya isikiwe katika njia kuu. Mwanzi uliopondeka hatauvunja, wala
utambi utokao moshi hatauzima; atatokeza hukumu kwa kweli.”
Huduma ya kimasihi mwanzi uliopondeka na utambi utokao moshi
Kimsingi Mwanzi uliopondeka na
utambi unaofuka moshi ulikuwa ni usemi uliotumika kuelezea pia kitu ambacho
kimepoteza maana, hakifai tena kwa matumizi, kitu kinachokwamisha kazi ya
uandishi kusonga mbele, lakini sio hivyo tu usemi huu ulitumika pia kuwaita
mataifa mengine wasio wayahudi yaani mataifa, hao waliitwa pia mwanzi
uliopondeka, na utambi utokao moshi ulimaanisha watu wa Mungu ambao wamepoteza
thamani yao, yaani walikuwa Nuru na sasa wamezimika hawafai tena kwa matumizi,
Mwanzi mataifa wasiofaa, Utambi wayahudi waliopoa.
Mwanzi uliopondeka – Uliwakilisha mataifa au watu wenye dhambi lakini
pia, walemavu au wagonjwa, watu wasio na matumaini, waliokandamizwa ambao kila
kitu kwao kimepoteza maana wamepoteza maana katika jamii, hawafai, wamevunjika,
hawana matumizi tena, ni wa kutupwa, wanyonge, waliochoka nafsi zao, sababu ya
changamoto, wenye laana, wenye mikosi wasioofaa kitu, wasio na uhakika wa
wokovu, wanaohesabika kuwa sio kitu wanaosubiria kuchomwa moto.
Utambi utokao moshi – Uliwakilisha watu wa Mungu Israel wenyewe
waliokuwa nuru lakini wamepoteza thamani wamepoa wamerudi nyuma, hawana thamani
tena ni watenda dhambi wamepoa, wote wanaosubiria hukumu yao tu hawana kitu cha
ziada zaidi ya kukwamisha kazi.
Isaya anaona kuwa wanasubiri
maamuzi ya hakimu ambaye ni Masihi, yeye anajua atawahukumuje hiki ndicho Isaya
alichokuwa anakiona katika unabii wake lakini anaona kama Masihi atakapokuja
huenda mambo yatakuwa tofauti, kwani hukumu zake ni tofauti na uweza wake ni
tofauti yeye Mwanzi uliopondeka hatauvunja, wala utambi utokao moshi hatauzima
kwa kuwa yeye ana Roho wa Mungu, anapendezwa na Mungu anajua atayatimiza vipi
mapenzi ya Mungu, Kwa Masihi hakutakuwa na mtu asiye na faida, hakutakuwa na
mtu wa kutupwa, au kuzimwa ni wakati wa uamsho mkubwa sana Masihi atatenda kwa
namna ya tofauti sana na mitazamo ya dini ya Kiyahudi
Huyu mataifa wanamtumainia,
Kimsingi Isaya aliyatabiri maswala hayo katika unabii wake na Kristo Yesu
alipokuja Duniani aliyatimiza haya na ndio Mathayo alipoyaona alikumbuka kile
alichokuwa amekitabiri nabii Isaya akaandika sawa na unabii wa Isaya
Mathayo 12:15-21 “Naye Yesu hali
akiyafahamu hayo akaondoka huko; na watu wengi wakamfuata; akawaponya wote,
akawakataza wasimdhihirishe; ili litimie neno lililonenwa na nabii Isaya,
akisema, Tazama, mtumishi wangu niliyemteua; Mpendwa wangu, moyo wangu
uliyependezwa naye; Nitatia roho yangu juu yake, Naye atawatangazia Mataifa
hukumu. Hatateta wala hatapaza sauti yake; Wala mtu hatasikia sauti yake njiani.
Mwanzi uliopondeka hatauvunja, Wala utambi utokao moshi hatauzima, Hata
ailetapo hukumu ikashinda. Na jina lake Mataifa watalitumainia.”
Masihi alipokuja alihukumu kwa
haki kwani kwanza aliwaona wote kuwa ni wenye dhambi, Mataifa na Wayahudi pia
na hakukuwa na aliye bora kuliko mwingine wote wanahitaji msaada wake, Wayahudi
na Mataifa mengine wote ni wenye dhambi wote wanamuhitaji Masihi hakuna mwenye
haki hata mmoja wala hakuna anayemtafuta Mungu wala hakuna anayetenda mema hata
mmoja wala hakuna anayemcha Mungu, hakuna aliye bora kuliko mwingine hakuna
mwenye nafuu wote wanahitaji rehema za Mungu na Masihi amekuja kwaajili hiyo
hakuja kuhukumu amaekuja kutangaza rehema za Mungu, amekuja kutangaza msamaha
wa dhambi, fadhili za Mungu na kuponya mwili na roho
Warumi 3:9-18 “Ni nini basi? Tu bora kuliko
wengine? La! Hata kidogo. Kwa maana tumekwisha kuwashitaki Wayahudi na Wayunani
ya kwamba pia wamekuwa chini ya dhambi; kama ilivyoandikwa, ya kwamba, Hakuna
mwenye haki hata mmoja. Hakuna afahamuye; Hakuna amtafutaye Mungu. Wote
wamepotoka, wameoza wote pia; Hakuna mtenda mema, la! Hata mmoja. Koo lao ni
kaburi wazi, Kwa ndimi zao wametumia hila. Sumu ya fira i chini ya midomo yao.
Vinywa vyao vimejaa laana na uchungu. Miguu yao ina mbio kumwaga damu.
Uharibifu na mashaka yamo njiani mwao. Wala njia ya amani hawakuijua. Kumcha
Mungu hakupo machoni pao.”
Huduma ya Masihi inatoa rehema
kwa wote waliovunjika na waliopoa wanaofuka moshi tu lakini moto umezimika wote
wanamuhitaji Yesu, achochee utambi uwake na aponye waliovunjika, uvumilivu na upole na upendo wa Bwana wetu
Yesu Kristo ndio unaowavumilia watu leo na kuwapa nafasi ili waponywe na moto
uwake tena, lakini sio hivyo tu Yesu yuko tayari kushughulika na wote
walioumizwa, wanaohitaji rehema na upendo wake yeye yuko tayari kuwahudumia na
kuwaponya watu wote wanapaswa kumuendea na watu wote wanapaswa kulitegemea jina
lake, Yeye hazimii wala hakati tamaa na mtu, watu wote watamtumainia na
kuliitia jina lake yeye yuko tayari kusaidia.
Matendo 4:10-12 “jueni ninyi nyote na watu
wote wa Israeli ya kuwa kwa jina la Yesu Kristo wa Nazareti, ambaye ninyi
mlimsulibisha, na Mungu akamfufua katika wafu, kwa jina hilo mtu huyu anasimama
ali mzima mbele yenu. Yeye ndiye jiwe lile lililodharauliwa na ninyi waashi,
nalo limewekwa kuwa jiwe kuu la pembeni. Wala hakuna wokovu katika mwingine
awaye yote, kwa maana hapana jina jingine chini ya mbingu walilopewa wanadamu
litupasalo sisi kuokolewa kwalo.”
Mwanzi uliopondeka na utambi utokao moshi.
Mathayo 12:15-21 “Naye Yesu hali
akiyafahamu hayo akaondoka huko; na watu wengi wakamfuata; akawaponya wote,
akawakataza wasimdhihirishe; ili litimie neno lililonenwa na nabii Isaya,
akisema, Tazama, mtumishi wangu niliyemteua; Mpendwa wangu, moyo wangu
uliyependezwa naye; Nitatia roho yangu juu yake, Naye atawatangazia Mataifa
hukumu. Hatateta wala hatapaza sauti yake; Wala mtu hatasikia sauti yake njiani.
Mwanzi uliopondeka hatauvunja, Wala utambi utokao moshi hatauzima, Hata
ailetapo hukumu ikashinda. Na jina lake Mataifa watalitumainia.”
Mathayo alipokuwa anawaona watu
mbalimbali matajiri kwa masikini, wenye nguvu na wasio na nguvu wakimiminika
kwa kutafuta msaada kwa Yesu alikumbuka kutimia kwa unabii wa Isaya na anaunukuu.
Huduma ya Masihi ilikazia ukweli
kuwa Yesu hakuja kwaajili ya wenye nguvu, wala wenye kujitosheleza,
wanaojifikiria kuwa wao ni wakamilifu amekuja kwaajlii ya waliovunjika wasio na
faida waliozimika, Yesu alitakasa wenye ukoma, aliwagusa wakoma waliokuwa
wamekataliwa, alisamehe wenye dhambi, aliwarejesha hata wale waliomkana mara
tatu kama Petro, alishughulika na wale ambao wangestahili kubadilishwa na
kutupwa, Mwanzi uliovunjika haukufaa tenza kwa waandishi zaidi ya kuchomwa moto
na kutumia mwingine na utambi uliofuka moshi ulisubiri kubadilishwa, Lakini
Masihi yeye angehuisha vile vinavyoonekana kutokufaa viweze kufaa kwa utukufu
wa Mungu
Luka 5:30-32 “Ikawa Mafarisayo na waandishi
wao kuwanung'unikia wanafunzi wake, wakisema, Mbona mnakula na kunywa pamoja na
watoza ushuru na wenye dhambi? Yesu akajibu akawaambia, Wenye afya hawana haja
na tabibu, isipokuwa walio hawawezi. Sikuja kuwaita wenye haki, bali wenye
dhambi, wapate kutubu.”
Marko 16:6-7 “Naye akawaambia, Msistaajabu;
mnamtafuta Yesu Mnazareti, aliyesulibiwa; amefufuka; hayupo hapa; patazameni
mahali walipomweka. Lakini enendeni zenu, mkawaambie wanafunzi wake, na Petro,
ya kwamba awatangulia kwenda Galilaya; huko mtamwona, kama alivyowaambia.”
Yohana 21:15-17 “Basi walipokwisha kula,
Yesu akamwambia Simoni Petro, Je! Simoni wa Yohana, wewe wanipenda kuliko hawa?
Akamwambia, Naam ,Bwana, wewe wajua kuwa nakupenda. Akamwambia, Lisha
wana-kondoo wangu. Akamwambia tena mara ya pili, Simoni wa Yohana, wanipenda?
Akamwambia, Ndiyo, Bwana, wewe wajua kuwa nakupenda. Akamwambia, Chunga kondoo
zangu. Akamwambia mara ya tatu, Simoni wa Yohana, wanipenda? Petro alihuzunika
kwa vile alivyomwambia mara ya tatu, Wanipenda? Akamwambia, Bwana, wewe wajua
yote; wewe umetambua ya kuwa nakupenda. Yesu akamwambia, Lisha kondoo zangu.”
Huduma ya kimasihi ni huduma ya
uponyaji wa mwili nafsi na roho, ni huduma ya uvumilivu ni huduma ya huruma na
upendo ni huduma ya kuchukuliana na ni
huduma ambayo haioni mkamilifu inaona kuwa kila mtu anahitaji huduma yake
isipokuwa wale wenye kiburi tu na wale wanaojihesabia haki, kila mtu na kila
mmoja anamuhitaji Bwana Yesu na ukarabati wa watu wa Mungu wa aina zote
unatakiwa kupatikana kanisani, kanisani sio mahali pa watakatifu tu ni mahali
pa watu wote wenye nguvu na dhaifu atakayekuja kuchuja ni Yesu mwenyewe, wajibu
wetu sisi ni kuhubiri injili, na kuwafundisha watu na Neno la Mungu lenyewe
litawabadilisha, Yesu mwenyewe atawaokoa na kuwasamehe watu wake yeye ndiye anayeweza
kuwafinyanga watu wake wakawa kama yeye alivyo, hukumu halali itatolewa siku ya
mwisho na mwenyewe sio sisi
Mathayo 13:47-50 “Tena ufalme wa mbinguni
umefanana na juya, lililotupwa baharini, likakusanya samaki wa kila namna; hata
lilipojaa, walilivuta pwani; wakaketi, wakakusanya walio wema vyomboni, bali
walio wabaya wakawatupa. Ndivyo itakavyokuwa katika mwisho wa dunia; malaika
watatokea, watawatenga waovu mbali na wenye haki, na kuwatupa katika tanuru ya
moto; ndiko kutakuwako kilio na kusaga meno.”
Uko uwezekano kuwa unaona ujumbe huu
huku ukiwa umevunjika moyo, una ndoa iliyovunjika, una uchumba uliovunjika una
mahusiano yaliyopondeka, una nuru iliyozimika una hasara katika biashara na
hujui utainukaje, una madeni, au utambi wako wa rohoni umezimika, matumaini ya
maisha yako na ndoto zako zimekwama mahali. Giza limetanda na kila kitu kinaonekana
kukwama katika maisha yako, uwezo wako wa kusimama tena umepotea, muda wako
umepotea, unajiuliza itakuwaje tena katika maisha yangu? Itakuwaje katika roho
yangu? Je naweza kusimama tena hata baada ya kuharibu namna hii? Lakini kwa
uwezo wa Bwana wetu Yesu Kristo, yeye anakuganga na kukuponya na kukuinua tena
nakuhakikishia moto uliozimika utawaka na moyo uliovunjika utainuka hii ndio
kazi ya Masihi amka leo acha kulia katika jina la Yesu Kristo mwana wa Mungu
aliye hai, Yesu alikuja kwaajili ya watu kama wewe watu ambao wanatarajiwa
kutupwa, na wanaoonekana kutokufaa katika jamii wenye matumaini yaliyofifia yeye
haogopi hayo na anatoa mwaliko kuwa watu wote wenye changamoto zozote zile waje
kwake
Mathayo 11:28-29 “Njoni kwangu, ninyi nyote
msumbukao na wenye kulemewa na mizigo, nami nitawapumzisha. Jitieni nira yangu,
mjifunze kwangu; kwa kuwa mimi ni mpole na mnyenyekevu wa moyo; nanyi mtapata
raha nafsini mwenu;”
“Maombi yangu yafike kwako Moyo,
uliopondeka hutadharau, Kiu yangu na haja yangu, nifanane nawe nifanane nawe,
nifanane nawe, Nifanye kama wewe, unifinyange, nifinyange, wakinitazama wakuone
wewe unifinyange, nifinyange”
Na. Rev. Innocent Samuel Kamote
Mkuu wa wajenzi mwenye Hekima!

.jpg)

