Mwanzo 26:19-22 “Watumwa wa Isaka
wakachimba katika lile bonde, wakapata kisima cha maji yanayobubujika.
Wachungaji wa Gerari wakagombana na wachungaji wa Isaka wakisema, Maji haya ni
yetu. Ndipo akakiita jina la kile kisima Eseki, kwa sababu waligombana naye.
Wakachimba kisima kingine, wakagombania na hicho tena. Akakiita jina lake
Sitna. Akaondoka huko akachimba kisima kingine, wala hicho hawakukigombania.
Akakiita jina lake Rehobothi, akasema, Kwa kuwa sasa BWANA ametufanyia nafasi,
nasi tutazidi katika nchi.”
Utangulizi:
Ni muhimu kufahamu kuwa mtu awaye
yote anapokuwa amebarikiwa na Mungu, au kama Mungu yuko pamoja na yeye anaweza
kupitia vipingamizi vya aina mbalimbali katika maisha, watu wa Mungu wakati
mwingine watapitia chuki zisizokuwa za kawaida, kuonewa wivu, na wakati
mwingine kupitia mapambano mengi, Maisha ya Isaka ni mojawapo ya mfano wa
matukio kama hayo, baada ya kuwa Mungu amemfungulia milango ya Baraka na uhuru,
kutoka katika kuandamwa na vita na chuki na wivu wa maisha kutoka kwa
wafilisti, Waligombania na kumpokonya visima vyake viwili yaani maji ya Eseki
na Stina, hatimaye alipata maji sehemu nyingine ambapo alipaita Rehoboth
akitangaza kwa imani kuwa sasa Bwana amemfanyia nafasi!, kwani kisima hicho
hakikugombaniwa tena.
Mwanzo 26:19-22 “Watumwa wa Isaka
wakachimba katika lile bonde, wakapata kisima cha maji yanayobubujika.
Wachungaji wa Gerari wakagombana na wachungaji wa Isaka wakisema, Maji haya ni
yetu. Ndipo akakiita jina la kile kisima Eseki, kwa sababu waligombana naye.
Wakachimba kisima kingine, wakagombania na hicho tena. Akakiita jina lake
Sitna. Akaondoka huko akachimba kisima kingine, wala hicho hawakukigombania.
Akakiita jina lake Rehobothi, akasema, Kwa kuwa sasa BWANA ametufanyia nafasi,
nasi tutazidi katika nchi.”
Leo tutachukua muda kujifunza na
kutafakari kwa kina kuhusiana na maisha ya Isaka ambayo kimsingi yanatufundisha
kuwa maisha ya watu wa Mungu na watu wa kawaida yana changamoto za aina
mbalimbali lakini hata hivyo tunapoendelea kumtegemea Mungu hatimaye Mungu
hutupa ahueni, tutajifunza somo hili Kwa
kuwa sasa Bwana ametufanyia nafasi kwa kuzingatia vipengele muhimu vitatu
vifuatayo:-
·
Maana ya
maneno Bwana ametufanyia nafasi
·
Maisha ya
changamoto za mtu wa Mungu
·
Kwa kuwa
sasa Bwana ametufanyia nafasi
Maana ya maneno Bwana ametufanyia nafasi.
Maneno Kwa kuwa Bwana ametufanyia
nafasi kwa Kiebrania “Rehoboth” yalitamkwa na Isaka yakimaanisha majira ya Mungu ya
kuwapa watu wake mpenyo, pumziko la kiroho, nafasi ya kukua, nafasi ya
kuongezeka, nafasi ya kuwa na Amani, nafasi ya kutokuweko katika migogoro,
nafasi ya kustawi pasipokuwa na upinzani, nafasi ya thamani na utulivu, kwa hiyo
neno “Rehoboth” au “Rechovoth” la Kiebrania lina maana ya
Nafasi kubwa, eneo la kukua na kupanuka, uhuru wa kutenda bila upinzani, nafasi
ya kustawi, na nafasi ya kuwa nje ya vikwazo, hali hii haisababishwi na akili
za kibinadamu bali inasababishwa na Mungu anapoingilia kati na kundoa shinikizo
na msongamano wa changamoto ili kutoa utulivu kwa watu wake, huu ni mchakato wa
kuondoka katika mashinikizo kadhaa ya maisha yanayopelekea kuifikia ndoto ya
utulivu unaohitajika kibinadamu.
Mungu alimpa nafasi Rehoboth
Yusufu baada ya mapito ya muda mrefu katika maisha kwa kusudi la kufikia hatima
yake - Mwanzo 41:38-41 “Farao akawaambia watumwa wake, Tupate wapi mtu kama huyu,
mwenye roho ya Mungu ndani yake? Farao akamwambia Yusufu, Kwa kuwa Mungu
amekufahamisha hayo yote, hapana mwenye akili na hekima kama wewe. Basi wewe
utakuwa juu ya nyumba yangu, na kwa neno lako watu wangu watatawaliwa. Katika
kiti cha enzi tu nitakuwa mkuu kuliko wewe. Farao akamwambia Yusufu, Tazama,
nimekuweka juu ya nchi yote ya Misri.”
Mungu alimpa nafasi Daudi nafasi
ya kutoka katika hali duni ya kuchunga kondoo na kudharaulika katika familia
mpaka kuwa mfalme katika Israel –
1Samuel 16:11-13 “Kisha Samweli akamwambia Yese,
Watoto wako wote wapo hapa? Naye akasema, Amesalia mdogo wao, na tazama,
anawachunga kondoo. Basi Samweli akamwambia Yese, Tuma watu, wamlete; kwa
sababu hatutaketi hata atakapokuja huku. Basi akatuma mtu, naye akamleta kwao.
Naye alikuwa mwekundu, mwenye macho mazuri, na umbo lake lilikuwa la kupendeza.
Bwana akasema, Ondoka, umtie mafuta; maana huyu ndiye.Ndipo Samweli akaitwaa
pembe yenye mafuta, akamtia mafuta kati ya ndugu zake; na roho ya Bwana
ikamjilia Daudi kwa nguvu tangu siku ile. Basi Samweli akaondoka, akaenda zake
Rama.”
Mungu anapokufanyia nafasi au kukuletea
“Rehoboth” anakuweka katika mahali
ambapo adui zako hawawezi kuzuia maendeleo na ustawi wako, Milango iliyokuwa
imefungwa au iliyokuwa inakutana na upinzani huanza kufunguka na kupata upenyo,
Milango ya Baraka huanza kutiririka kwa urahisi, miguu yako inawekwa mahali palipoinuka
na hakuna taabu tena ya kupita katika mabonde
Zaburi 31:7-8 “Na nishangilie, nizifurahie
fadhili zako, Kwa kuwa umeyaona mateso yangu. Umeijua nafsi yangu taabuni, Wala
hukunitia mikononi mwa adui; Miguu yangu umeisimamisha panapo nafasi.”
Maisha ya changamoto za mtu wa Mungu
Kabla Isaka hajapata utulivu wa
maisha “Rehoboth” alipitia
changamoto nyingi sana ambazo wakati mwingine hata watu wengine wa Mungu
wanapitia, hii inamaanisha kuwa changamoto ni sehemu ya kawaida ya maisha ya
mwanadamu lakini hata hivyo tukimtegemea Mungu atajitokeza hatimaye na
kutupatia nafasi
·
Isaka
alipoteza mama yake mpendwa Sara - Jambo
hili liliumiza sana maisha yake kama wote tunavyofahamu unapoondokewa na
wazazi, moyo unauma sana na unagubikwa na upweke mkubwa hata hivyo ujio wa Rebeka katika maisha ya
Isaka ulimpa unafuu katika changamoto hiyo
Mwanzo 24:67 “Isaka
akamwingiza Rebeka katika hema ya mama yake, Sara, akamtwaa Rebeka, akawa
mkewe, akampenda; Isaka akafarijika kwa ajili ya kufa kwa mamake.”
·
Isaka
alipitia kipindi cha kukosa mtoto miaka 20 – Baada ya Rebeka kuwa faraja
kwa muda sasa wanakutana na changamoto nyingine katika maisha na sasa wanakosa
mtoto kwa muda wa miaka 20, Isaka alimuoa Rebeka akiwa na miaka 40 na alikuja
kupata watoto Esau na Yakobo akiwa na miaka 60, hiki ni kipindi cha kupimwa
imani na uvumilivu, na ni mpaka Isaka alipomuomba Mungu ndipo Mungu alipojibu maombi
na watoto mapacha wakapatikana
Mwanzo 25:19-28 “Na
hivi ndivyo vizazi vya Isaka, mwana wa Ibrahimu. Ibrahimu alimzaa Isaka. Isaka
akawa mwenye miaka arobaini alipomtwaa Rebeka binti Bethueli, Mshami, wa
Padan-aramu, ndugu wa Labani, Mshami, kuwa mke wake. Isaka akamwomba BWANA kwa
ajili ya mke wake, maana alikuwa tasa. Naye BWANA akamwitikia, na Rebeka mkewe
akachukua mimba. Watoto wakashindana tumboni mwake. Naye akasema, Ikiwa ni
hivi, kuishi kwanifaa nini? Akaenda kumwuliza BWANA. BWANA akamwambia, Mataifa
mawili yamo tumboni mwako, Na kabila mbili za watu watafarakana tangu tumboni mwako.
Kabila moja litakuwa hodari kuliko la pili, Na mkubwa atamtumikia mdogo. Siku
zake za kuzaa zilipotimia, tazama! Mapacha walikuwamo tumboni mwake. Wa kwanza
akatoka, naye alikuwa mwekundu mwili wote kama vazi la nywele. Wakamwita jina
lake Esau. Baadaye ndugu yake akatoka, na mkono wake unamshika Esau kisigino.
Akaitwa jina lake Yakobo. Isaka alikuwa mwenye miaka sitini mkewe alipowazaa.
Watoto wakakua, Esau alikuwa mtu ajuaye kuwinda wanyama, mtu wa nyikani, na
Yakobo alikuwa mtu mtulivu, mwenye kukaa hemani. Basi Isaka akampenda Esau, kwa
sababu alikula mawindo yake, na Rebeka akampenda Yakobo.”
·
Isaka
alikabiliwa na njaa kubwa katika inchi – Akiwa katika nchi ya ahadi Isaka
anakumbwa na njaa kali sana, njaa kama ya siku za baba yake Abrahamu ambayo ilimpelekea
Abrahamu kukimbilia Misri hata hivyo kwa neema ya Mungu, Mungu alisema na Isaka
asishuke kwenda Misri kama ilivyokuwa kwa baba yake, Mungu aliamua kumbariki
pale pale mahali ambapo wengine walikuwa
hawana matumaini.
Mwanzo 26:1-5 “Ikawa
njaa katika nchi hiyo, mbali na njaa ile ya kwanza iliyokuwa siku za Ibrahimu.
Isaka akamwendea Abimeleki, mfalme wa Wafilisti, huko Gerari. BWANA akamtokea,
akasema, Usishuke kwenda Misri, kaa katika nchi nitakayokuambia. Kaa ugenini
katika nchi hiyo, nami nitakuwa pamoja nawe, na kukubariki, maana nitakupa wewe
na uzao wako nchi hizi zote. Nami nitakifanya imara kiapo nilichomwapia
Ibrahimu baba yako. Nitazidisha uzao wako kama nyota za mbinguni, nami nitawapa
uzao wako nchi hizi zote, na katika uzao wako mataifa yote ya dunia
watajibarikia. Kwa sababu Ibrahimu alisikia sauti yangu, akayahifadhi maagizo
yangu, na amri zangu, na hukumu zangu, na sheria zangu.”
·
Isaka
alikabiliwa na kuonewa wivu (Husuda) na wafilisti – Mungu alimbariki sana
Isaka baada ya kubaki katika inchi ya Mkanaani, Mungu alikuwa amemuwezesha
Isaka kuchimba visima vya baba yake Ibrahimu na kumsaidia kwa kutumia maji
yanayobubujika kufanya kilimo cha umwagiliaji na kujipatia mazao na kuwanywesha
mifugo hivyo kukawa na mafanikio makubwa sana hata wakati wa njaa Isaka
alipanda kipimo cha mbegu na kuvuna mara mia, hivyo mtu huyu akawa mkuu mno na
hapo ndipo Wafilisti wakamuonea wivu, kumbe kadiri Mungu anavyokubariki sana na
kukuinua juu ndivyo Baraka zako zinavyoambatana na upinzani kutoka kwa watu
wenye wivu wenye uchungu
Mwanzo 26:12-14 “Isaka
akapanda mbegu katika nchi ile, akapata mwaka ule vipimo mia kwa kimoja, BWANA
akambariki. Na mtu huyu akawa mkuu, akazidi kusitawi, hata akawa mkuu sana.
Akawa na mali ya kondoo, na mali ya ng'ombe, na watumwa wengi. Hao Wafilisti
wakamhusudu.”
·
Isaka
alipambana na jaribu la kufukiwa kwa visima vyake – Bila shaka wafilisti
walibaini kuwa utajiri wa Isaka na mafanikio makubwa aliyokuwa nayo ni uwepo wa
Mungu na vile vile visima alivyokuwa amechimba na vikawa vinabubujisha maji, Wafilisti
waliamua kuvifukia visima vyote ambavyo kimsingi vilikuwa vya baba yake
yaani Abrahamu, Wafilisti walivifukia, wakati wote shetani atataka kufukia kila
chanzo cha Baraka kwa watu wa Mungu ili usitoke
Mwanzo 26:15-21 “Na
vile visima vyote walivyochimba watumwa wa baba yake, siku za Ibrahimu babaye,
Wafilisti walikuwa wamevifukia, wakavijaza kifusi. Abimeleki akamwambia Isaka,
Utoke kwetu, maana wewe una nguvu sana kuliko sisi. Basi Isaka akatoka huko
akapiga kambi katika bonde la Gerari, akakaa huko.Isaka akarudi akavichimbua
vile visima vya maji walivyovichimba siku za Ibrahimu babaye; maana wale
Wafilisti walikuwa wamevifukia baada ya kufa kwake Ibrahimu; naye akaviita
majina kufuata majina alivyoviita babaye.Watumwa wa Isaka wakachimba katika
lile bonde, wakapata kisima cha maji yanayobubujika. Wachungaji wa Gerari
wakagombana na wachungaji wa Isaka wakisema, Maji haya ni yetu. Ndipo akakiita
jina la kile kisima Eseki, kwa sababu waligombana naye. Wakachimba kisima
kingine, wakagombania na hicho tena. Akakiita jina lake Sitna.”
·
Isaka
alifukuzwa kwa sababu ua ukuu wake - Isaka
alibarikiwa sana na kuwa mtu mkubwa sana, uwepo wa Mungu ulikuwa pamoja naye,
upako na karama zilikaa juu yake, hakuwa mtu wa vita alikuwa mtu wa utulivu na
mtu wa Amani lakini hata hivyo adui zake walishindwa kumstahimili na hivyo
waliamua kumfukuza, ziko nyakati ambazo unaweza kukataliwa bila sababu au
unaweza kutengenezewa zengwe ili usiwepo katika maeneo hayo na sababu kubwa
watu wanadhani ukuu wako unatokana na hapo ulipo, lakini sio hivyo tu watu wema
wakati mwingine hukataliwa na hata kuuawa kwa sababu ya wema wao
Mwanzo 26:13-16 “Na
mtu huyu akawa mkuu, akazidi kusitawi, hata akawa mkuu sana. Akawa na mali ya
kondoo, na mali ya ng'ombe, na watumwa wengi. Hao Wafilisti wakamhusudu. Na
vile visima vyote walivyochimba watumwa wa baba yake, siku za Ibrahimu babaye,
Wafilisti walikuwa wamevifukia, wakavijaza kifusi. Abimeleki akamwambia Isaka,
Utoke kwetu, maana wewe una nguvu sana kuliko sisi.”
·
Isaka
alinyimwa nafasi – Mgogoro wa visima pamoja na kufukuzwa katika nchi ya
Wafilisti wakati wote ilikuwa inalenga kumnyima Isaka ustawi, adui alikuwa
anawekwa vikwazo ili kumnyima Isaka fursa ya utulivu na mafanikio, waligombea
kisima cha kwanza akakiita Eseki
maana yake UGOMVI, walifukia kisima cha
pili na kukigombea akakiita Sitna
maana yake UADUI kwa hiyo utaona
Isaka anakabiliwa na ugomvi, uadui, upinzani, chuki na husuda, lakini kwa jinsi
alivyokuwa muungwana na mwororo, hakugombana na mtu, tunajifunza ya kuwa
tunaweza kushinda vita vingi kwa kuwa waungwana na kwa kutumia hekima kuliko
kushindana na kujiingiza kwenye migogoro, kutokana na utulivu huu hatimaye
Mungu aliamua kumpa utulivu halisi na hapa ndipo Bwana alipompa Nafasi, Rehoboth
Mwanzo 26:17-22 “Basi
Isaka akatoka huko akapiga kambi katika bonde la Gerari, akakaa huko. Isaka
akarudi akavichimbua vile visima vya maji walivyovichimba siku za Ibrahimu
babaye; maana wale Wafilisti walikuwa wamevifukia baada ya kufa kwake Ibrahimu;
naye akaviita majina kufuata majina alivyoviita babaye. Watumwa wa Isaka
wakachimba katika lile bonde, wakapata kisima cha maji yanayobubujika.
Wachungaji wa Gerari wakagombana na wachungaji wa Isaka wakisema, Maji haya ni
yetu. Ndipo akakiita jina la kile kisima Eseki, kwa sababu waligombana naye.
Wakachimba kisima kingine, wakagombania na hicho tena. Akakiita jina lake
Sitna. Akaondoka huko akachimba kisima kingine, wala hicho hawakukigombania.
Akakiita jina lake Rehobothi, akasema, Kwa kuwa sasa BWANA ametufanyia nafasi,
nasi tutazidi katika nchi.”
Kwa kuwa sasa Bwana ametufanyia nafasi
Mpenzi maisha ya Isaka yanamkumbusha kila mmoja wetu kuwa changamoto
unazozipitia ni za kawaida, kila mtu wa Mungu anaweza kupitia changamoto za
iana mbalimbali katika maisha, Yesu alisema ulimwenguni mnayo dhiki, kwa sababu
hiyo dhiki kama hizi ni za kawaida kwa watu wa Mungu, hata hivyo tunapoendelea
kuwa na subira na kumtegemea Mungu hatimaye Mungu atatufanyia nafasi REHOBOTH Isaka kwa kweli hakuzitegemea
akili zake mwenyewe, tunaweza kukiri kuwa kweli alikuwa na taaluma ya kuchimba
visima lakini taaluma hiyo ingeweza kuigizwa na wengine au kusambazwa lakini
hii ilikuwa ni ishara ya kuwa Mungu alikuwa pamoja naye, ukiri wake na kauli
yake haikuwa kuwa sasa tumetoboa na badala yake alikiri kuwa ni Mungu ndiye
aliyewafanyia nafasi. Isaka aliendelea
kubarikiwa mpaka adui zake walikuja kujipendekeza na kufanya Amani naye huku
wakitambua kuwa hakika alikuwa na Mungu
Mwanzo 26:22-29 “Akaondoka huko akachimba
kisima kingine, wala hicho hawakukigombania. Akakiita jina lake Rehobothi,
akasema, Kwa kuwa sasa BWANA ametufanyia nafasi, nasi tutazidi katika nchi.
Akapanda kutoka hapo mpaka Beer-sheba. BWANA akamtokea usiku uleule, akasema,
Mimi ni Mungu wa Ibrahimu baba yako, usiogope, maana mimi ni pamoja nawe, nami
nitakubarikia, na kuzidisha uzao wako kwa ajili ya Ibrahimu mtumishi wangu.
Akajenga madhabahu huko, akaliitia jina la BWANA. Akapiga hema yake huko, na
watumwa wa Isaka wakachimba kisima huko. Ndipo Abimeleki akamwendea kutoka
Gerari, pamoja na Ahuzathi rafiki yake, na Fikoli, jemadari wa jeshi lake. Isaka
akawauliza, Mbona mwanijia, nanyi mmenichukia, mkanifukuza kwenu?Wakasema,
Hakika tuliona ya kwamba BWANA alikuwa pamoja nawe; nasi tukasema, Na tuapiane,
sisi na wewe, na kufanya mapatano nawe ya kuwa hutatutenda mabaya, iwapo sisi
hatukukugusa wewe, wala hatukukutendea ila mema, tukakuacha uende zako kwa
amani; nawe sasa u mbarikiwa wa BWANA.”
Mambo ya kujifunza kutokana na maisha ya Isaka hapo:-
1. Mungu ndiye anayetengeneza nafasi – Isaka
hakusema kwamba tumetoboa, au tumewapiga bao Wafilisti au hawatuwezi hapana,
yeye alisema sasa Bwana ametufanyia nafasi na tutazidi kuongezeka alisema haya
kutokana na amani kwamba sasa maadui waliogopa kumfuatilia, dhamiri zao
ziliwashitaki kwamba wataendelea na dhuluma zao mpaka lini mafanikio ya kweli
ni yale ambayo Bwana ndiye anayekupigania, adui zako wanatamani usiwepo lakini
wewe unaendelea kustawi na sababu ya ustawi wako inagunduliwa wazi kuwa ni
Mungu, Mungu akikuandalia mazingira inapendeza sana kuliko wewe mwenyewe
ukijilazimishia mazingira ya mafanikio
Zaburi 127:1 “Bwana asipoijenga nyumba Waijengao wafanya kazi bure.
Bwana asipoulinda mji Yeye aulindaye akesha bure.”
2. Mafanikio ya kweli yanahitaji uvumilivu – wako
watu ambao wanatamaa ya mafanikio na wanadhani kuwa mafanikio yanakuja kwa
kuamka tu asubuhi, au kwa kuyalazimisha, nimeona watu wengi sana hasa vijana
wanataka kila kitu kitokee kwa haraka lakini ni muhimu kuwa wavumilivu na kuwa
wenye subira kwa sababu Mungu sio dhalimu kwa wakati wake atafanya, Isaka
alivumilia, dhihaka, utasa, huzuni, njaa, wivu, ugomvi, kufukuzwa, uadui, dhuluma
na kadhalika, alikuwa na nguvu kubwa sana lakini hakuitumia kupigana na adui
zake na kisha Bwana mwenyewe alimfanyia
nafasi, hatupaswi kujipigania, hatupawi kukata tamaa hata kama Eseki na Sitna
zitatokea katika maisha yetu hatimaye REHOBOTH italetwa na Bwana kila mtu wa Mungu ajifunze ya kuwa anahitaji
uvumilivu Saburi na mambo hayatakuja
kuwa wakati mwingine kwa haraka kama tunavyofikiri
3.
Mungu
anapokufungulia mlango Rehoboth - anakutengenezea mazingira ya kuongezeka,
anakufanya ukue, huduma yako itakua, familia yako itaongezeka, uchumi wako
utakuwa, Kiroho utakuwa, ushawishi utaiongezeka
utaogopwa, utaabudu kwa Amani na usalama, utafutwa machozi, adui zako
watakuja kupatana na wewe wao wenyewe, utafurahia ndoa yako, utamfurahia Bwana
Mungu wako, utafurahia biashara zako, utafurahia mifugo na kilimo, utaongeza
maarifa hekima na elimu, utatimiza makusudi ya Mungu utakuwa na shuhuda,
utatumika
Zaburi 4:1-5 “Ee Mungu wa haki yangu, uniitikie niitapo; Umenifanyizia
nafasi wakati wa shida; Unifadhili na kuisikia sala yangu. Enyi wanadamu, hata
lini utukufu wangu utafedheheka? Je! Mtapenda ubatili na kutafuta uongo? Bali
jueni ya kuwa Bwana amejiteulia mtauwa; Bwana atasikia nimwitapo. Mwe na hofu
wala msitende dhambi, Tafakarini vitandani mwenu na kutulia. Toeni dhabihu za
haki, Na kumtumaini Bwana”
Ndugu zangu wapenzi kaka zangu na
dada zangu, haijalishi ni maisha ya namna gani unayapitia, tambua tu kuwa dunia
haina huruma hata kidogo na maisha yako, ni lazima umuwekee Mungu tumaini lako,
unapojikita katika kumtegemea Mungu na kujiepusha na migogoro kisha wewe kuwa
sababu ya Amani Mungu wa Ibrahimu, na wa Isaka na Yakobo baba zetu hatatuacha
dunia yote na kila mtu anayesikia shuhuda zako atajua wazi kuwa Bwana yuko
pamoja nawe, Bwana atakupigania nawe utanyamaza kimya, adui zako watakuja
kukusujudia, hiki ndicho kilichomtokea Isaka Bwana alikuwa pamoja naye mpaka
adui zake walilitambua hilo na kufanya Amani naye, wewe hupigani mwenyewe yuko
anayekupigania naye yu hai katika jina la Yesu Kristo mwana wa Mungu aliye hai,
Amen!
Na. Rev. Innocent Samuel Kamote.
Mkuu wa wajenzi mwenye Hekima.


