Ijumaa, 11 Oktoba 2024

Je ninyi nanyi mwataka kuondoka?


Yohana 6:65-69 “Akasema, Kwa sababu hiyo nimewaambia ya kwamba hakuna mtu awezaye kuja kwangu isipokuwa amejaliwa na Baba yangu. Kwa ajili ya hayo wengi miongoni mwa wanafunzi wake wakarejea nyuma, wasiandamane naye tena. Basi Yesu akawaambia wale Thenashara, Je! Ninyi nanyi mwataka kuondoka? Basi Simoni Petro akamjibu, Bwana! Twende kwa nani? Wewe unayo maneno ya uzima wa milele. Nasi tumesadiki, tena tumejua, ya kuwa wewe ndiwe Mtakatifu wa Mungu.”




Utangulizi:

Je kuna watu wamewahi kukuacha na kuondoka katika maisha yako? Je kuna watu hawakupigii simu wala hawashughuliki tena na maisha yako? Je kuna watu mlikuwa karibu sana na siku hizi hawako karibu kama ilivyokuwa zamani? Je unahuzunika kwaajili yao? Je unalalamika kuwa hawakusalimii, hawatumi hata ujumbe na hawaulizi hata uko wapi na unafanya nini?, hawashughuliki hata kukusalimu?  kuna watu ulikuwa msaada mkubwa sana kwao, lakini sasa wako mbali na wewe? Je unahuzunika kwaajili yao? Kuna watu walikuwa faraja kubwa sana katika maisha yako, uliwapenda na wao wakakupenda, wakakufuata lakini sasa ni kama hawako na wewe, kuna wale mlisoma nao shule moja, darasa moja, kuna wale uliwasimamia harusi, kuna wale mlikuwa pamoja, mlicheza pamoja, kuna wale walikaa kwenu wakasomea kwenu, kuna wale ulisoma kwao ukakulia kwao, kuna wale ulikuwa msaada mkubwa kwao kiroho na kimwili na sasa ni kama hawataki kutambua mchango wako je unaumia kwaajili yao? Unalia kwaajili yao? Unasikitia kwaajili yao? Sikiliza wako watu ambao Mungu huwavuta kwetu na kuwaleta karibu nasi kwa makusudi maalumu, wako ambao Mungu amewaleta kwetu kama wenzi wetu, ndugu zetu, watoto wetu na ambao tunawafurahia hawa ni furaha yetu ni damu yetu ni watiifu kwetu hawawezi kutuacha kwa sababu Mungu alikusudia wawe nasi milele, kwa wakati mzuri na wakati mbaya, wako pamoja nasi hawana namna ya kujitoa kwetu, wao ni familia hawawezi kutuacha wala sisi hatuwezi kuwaacha. Lakini wako ambao Mungu huwaleta kwetu kwa sababu maalumu kama marafiki kwa kitambo, ni watu wema kwetu na wazuri kwetu lakini uko wakati ambao Mungu hufunga mlango na kuwaacha waende zao kwa sababu hawana shughuli kwetu tena, lile kusudi ambalo Mungu alikuwa amelikusudia kwa kuwaleta kwetu limeisha, Mlango umefungwa kwao kwaajili yetu, hawawezi tena kwenda unakoenda kwa hiyo Mungu hufunga mlango kwaajili yao, mchango wao wa kimwili na kiroho na kiushirika unakuwa umeishia hapo ambapo Mungu amekusudia uishie, huu ni ukweli ulio mchungu katika maisha, lakini hatuna budi kuukubali na kuujifunza na kujua kuwa ni mapenzi ya Mungu., Kama wana kazi nasi Mungu atawaleta tena Mara.

Muhubiri 3:1-8 “Kwa kila jambo kuna majira yake, Na wakati kwa kila kusudi chini ya mbingu. Wakati wa kuzaliwa, na wakati wa kufa; Wakati wa kupanda, na wakati wa kung'oa yaliyopandwa; Wakati wa kuua, na wakati wa kupoza; Wakati wa kubomoa, na wakati wa kujenga; Wakati wa kulia, na wakati wa kucheka; Wakati wa kuomboleza, na wakati wa kucheza; Wakati wa kutupa mawe, na wakati wa kukusanya mawe; Wakati wa kukumbatia, na wakati wa kutokumbatia; Wakati wa kutafuta, na wakati wa kupoteza; Wakati wa kuweka, na wakati wa kutupa; Wakati wa kurarua, na wakati wa kushona; Wakati wa kunyamaza, na wakati wa kunena; Wakati wa kupenda, na wakati wa kuchukia; Wakati wa vita, na wakati wa amani.”

Leo tutachukua muda kujifunza kwa kina na mapana na marefu kuhusiana na uhusiano uliofifia au uliokufa au ulioondoka na faida zake katika ufalme wa Mungu, tutajifunza namna unavyoweza kuelewa Mapenzi ya Mungu watu wanapokuacha na kuondoka zao katika maisha yako, Utajifunza namna na jinsi unavyopaswa kutokuhuzunika na kuwa na mashaka watu wanapokuacha na kukuona huna maana kwao, na kuona ya kuwa hawakuhitaji tena, hupaswi kulazimisha, wala hupaswi kujikomba komba, wewe umeumbwa kwa thamani kubwa sana  na; Ni Mungu tu aliyekuumba ndiye anayeijua thamani yako, kwa hiyo hatujifunzi kubomoa uhusiano hapa katika somo hili lakini tunajifunza kuwaachia watu wanaojiondoa katika maisha yetu wajiondoe, wataendelea kuwa rafiki zetu, na tutaendelea kuwapenda, lakini kama hawajihusishi na maisha yetu hatupaswi kuumia lazima ufikie wakati ukubali waende na ujue ya kuwa Mungu ameruhusu waende zao!, na kuna faida zake katika hilo, kwa hiyo hupaswi kulazimisha wakae, kwani unapojaribu kulazimisha kuwa na watu ambao wameshajiondoa katika maisha yako au Mungu amewaondoa katika maisha yako hii maana ni nini? Maana yake yake unajaribu kung’ang’ania, na kulazimisha kitu ambacho, Mungu ameshamalizana nacho katika maisha yako!, fahamu kuwa kila mtu ambaye Mungu alimleta kwako alimleta yeye kwa kusudi la kukujenga na kukupa changamoto na unapofika wakati mtu huyo au watu hao wanaondoka fahamu kuwa ni Mungu amewaondoa kwako kwa kusudi maalumu, kwa hiyo hupaswi kushangaa, kulalamika au kujifikiri kuwa una mapungufu na kulalamika na kuhuzunika na kulaani hapana!

Kifungu kile cha msingi tulichokisoma leo, ndicho ambacho kinabeba mafunuo yote ambayo Mungu amekusudia kutufundisha katika siku ya leo kwa mfumo wa kichambuzi (an Expository preachings) na tutakiangalia kupitia mstari kwa mstari tukizingatia vipengele husika katika somo hili hebu tukisome tena na kisha tutakifanyia uchambuzi wake

Yohana 6:65-69 “Akasema, Kwa sababu hiyo nimewaambia ya kwamba hakuna mtu awezaye kuja kwangu isipokuwa amejaliwa na Baba yangu. Kwa ajili ya hayo wengi miongoni mwa wanafunzi wake wakarejea nyuma, wasiandamane naye tena. Basi Yesu akawaambia wale Thenashara, Je! Ninyi nanyi mwataka kuondoka? Basi Simoni Petro akamjibu, Bwana! Twende kwa nani? Wewe unayo maneno ya uzima wa milele. Nasi tumesadiki, tena tumejua, ya kuwa wewe ndiwe Mtakatifu wa Mungu.”

Tutajifunza somo hili “Je ninyi nanyi mwataka kuondoka?” kwa kuzingatia vipengele vitatu vifuatavyo:-

 

·         Mungu ndiye mwanzilishi wa uhusiano.

·         Maumivu ya kuvunjika kwa uhusiano.

·         Je ninyi nanyi mwataka kuondoka?

 

Mungu ndiye mwanzilishi wa uhusiano

Yohana 6:65 “Akasema, Kwa sababu hiyo nimewaambia ya kwamba hakuna mtu awezaye kuja kwangu isipokuwa amejaliwa na Baba yangu.”

Katika kifungu hiki Yesu Kristo anatufunulia jambo ambalo sio tu linatokea katika maisha yake lakini vile vile linatokea katika maisha yetu kama watoto wa Mungu, Yesu alizungumza hili kuhusiana na wanafunzi wake akieleza kuwa hakuna mtu awezaye kuja kwake isipokuwa amejaliwa na baba yake wa Mbinguni, hili linatufunualia sisi nasi kuwa Ni Mungu ndiye anayeruhusu watu watukaribie na ni Mungu ndiye anayeruhusu watu waondoke,  Marafiki zetu wanaweza kuwa msaada mkubwa sana katika maisha yetu, wanaweza kutumiwa na Mungu kututia moyo, kutusaidia, kutujenga na kutupa ufahamu fulani katika safari zetu za kiroho na kimwili na kisaikolojia na kimakuzi, kwa hiyo marafiki ni neema ya Mungu, ni kupitia mahusiano ya kirafiki Mungu huwatumia marafiki kutuonyesha upendo, kutuonyesha namna na jinsi Mungu anavyojali, na hata kututia moyo na wakati mwingine huwatumia kutupa changamoto, kwa hiyo kila urafiki ni lazima utunzwe na kuchukuliwa kama zawadi ya Mungu katika maisha yetu na kuwa kupitia wao liko kusudi la Mungu, marafiki wengine huokoa maisha yetu kutoka katika maangamizi ya adui, wengine hutufundisha kuwa hata kama wako watu wanatuchukia bado wako ambao wanatuthamini sana na wanathamini mchango wetu na umuhimu wetu katika dunia hii, wengine hutusaidia kukua kiroho, na wengine tunawasaidia wao kukua kiroho na kadhalika kwa ujumla tunahitajiana na ndio maana tunahitaji ushirika.

1Samuel 18:1-5 “Ikawa Daudi alipokwisha kusema na Sauli, roho ya Yonathani, ikaambatana na roho ya Daudi, Yonathani akampenda kama roho yake mwenyewe. Sauli akamtwaa siku ile, wala hakumwacha arudi tena nyumbani kwa baba yake. Nao Yonathani na Daudi wakaahidiana, kwa kuwa alimpenda kama roho yake mwenyewe. Ndipo Yonathani akalivua joho alilokuwa amelivaa, akampa Daudi, na mavazi yake, hata na upanga wake pia, na upinde wake, na mshipi wake. Basi Daudi akatoka kwenda kila mahali alikotumwa na Sauli, akatenda kwa akili; Sauli akamweka juu ya watu wa vita; jambo hili likawa jema machoni pa watu wote, na machoni pa watumishi wa Sauli pia.”

Daudi hakukubalika sana kwa Sauli lakini hata hivyo mwana wa mfalme Yonathan alikuwa rafiki mwenye kufaa sana kwa Daudi, maandiko yanaeleza kuwa Yonathan alimkubali Daudi na na watu hawa walikuwa na agano la urafiki uliodumu sana hata baada ya maisha yao, ulikuwa ni urafiki wa kweli na wenye kufaa sana, ulikuwa ni urafiki wenye uhusiano wa kina kama uhusiano wa ndugu, Yonathan alikuwa mwelewa kwa rafiki yake Daudi, Yonathan aliyajua mapenzi ya Mungu yaliyokuwa juu ya Daudi, Yonathan hakuwa rafiki mwenye wivu wala hila, Yonathan alimtia moyo Daudi, alimpa mavazi ya kifalme aliyotumia mwenyewe, alimpa silaha, alimlinda alikuwa akimtakia mema, pamoja na kuwa baba wa Jonathan hakumpenda Daudi, alimchukia alimkusudia mabaya lakini haikuwa hivyo kwa Yonathan yeye alikuwa rafiki wa kweli. Na mtu ambaye aliangalia maslahi ya Mungu kwa upana. Hakuwahi kumponda wala kumchafulia sifa yake wala kutaka rafiki yake asipate kibali kwa mfalme, wakati wote Yonathan alikuwa faraja kubwa

1Samuel 19:4-6 “Naye Yonathani akamsifu Daudi kwa Sauli, babaye akamwambia, Mfalme asikose juu ya mtumishi wake, yaani, juu ya Daudi kwa maana yeye hakukosa juu yako, tena matendo yake kwako yamekuwa mema sana. Kwa kuwa alitia uhai wake mkononi mwake, na kumpiga yule Mfilisti, naye Bwana akawatendea Israeli wote wokovu mkuu. Wewe mwenyewe uliona jambo hilo, ukafurahi; basi kwa nini kukosa juu ya damu isiyo na hatia, umwue huyo Daudi bure?Sauli akaisikiliza sauti ya Yonathani; naye Sauli akaapa, Aishivyo Bwana, yeye hatauawa.”

Kwa ujumla Yonathan alikuwa rafiki wa kweli kwa Daudi, alikuwa ni zaidi ya ndugu, alilinda uhai wa Daudi, na hakukubali maisha ya Daudi yawe hatarini wakati wote alitengeneza mazigira mazuri, ili raiki yake akubalike kwa baba yake asionekane kuwa muhalifu, alimtetea na kumtia Moyo na alimjulisha kuhusu hatari ambazo zingeweza kumkabili, kama tunataka kujifunza watu waliokuwa na urafiki wa dhati basi Daudi na Yonathani ni mfano wa kuigwa, Yonathani alikuwa ni rafiki aliyeambatana na Daudi na mwenye kufaa sana kuliko ndugu.

Mithali 18:24 “Ajifanyiaye rafiki wengi ni kwa uangamivu wake mwenyewe; Lakini yuko rafiki aambatanaye na mtu kuliko ndugu.”              

Marafiki zetu hawaji wenyewe kwetu huwa tunaletewa na Mungu na Mungu ndiye anayewavuta watu kuja kwetu, kama vile tu alivyowavuta wanafunzi kuja kwa Yesu Kristo, hakuna mtu awezaye kuja kwangu, isipokuwa amejaliwa na Baba yangu, Neno hilo kujaaliwa katika kiyunani linatumika neno “Didōmi” kimatamshi ni Did-o-mee ambalo maana yake “with the palm of hand” yaani ni tendo la Mungu kuushika mkono na kumleta mtu moja kwa moja na kushikisha katika kiganja cha mkono wa mwingine kama tu vile mtu anayemkabidhi bibi harusi kwa mumewe siku ya harusi yake, kwa hiyo Ni Mungu Baba ndiye anayetushika mkono na kutupeleka katika mikono ya Yesu, hali kadhalika ni Mungu ndiye anayewashika mkono wale waliokusudiwa kuwa rafiki zetu na kuwaleta katika mikono yetu, Kwa hiyo ni muhimu sana kutomchukulia kwa dharau mtu awaye yote anayetamani kuwa na urafiki na wewe kwa sababu kila unayeletewa au anayekujia analetwa kwako na Mungu kwa kusudi maalumu katika maisha yako na kwa ufalme wa Mungu, wakati wote watu wanapokuwa marafiki mioyo yao inaunganishwa kuwa kitu kimoja kwaajili ya mafanikio ya yule ambaye Mungu amemkusudia au kwa kufaidiana, na kila wakati Mungu huhakikisha kuwa pande zote mbili zinanufaika na urafiki huo, kwa hiyo wote mnajengana na kufaidiana kwani chuma hunoa chuma Mithali 27:17 “Chuma hunoa chuma; Ndivyo mtu aunoavyo uso wa rafiki yake.” Marafiki zetu huletwa kwetu na Mungu kwa kusudi la kutusaidia na sisi kuwasaidia na wakati mwingine kwajili ya kufaidiana, kama Barnaba na Sauli au Paulo

Matendo 9:26-28 “Na Sauli alipofika Yerusalemu, alijaribu kujiunga na wanafunzi, nao walikuwa wakimwogopa wote, wasisadiki ya kuwa yeye ni mwanafunzi. Lakini Barnaba akamtwaa, akampeleka kwa mitume, akawaeleza jinsi alivyomwona Bwana njiani, na ya kwamba alisema naye, na jinsi alivyohubiri kwa ushujaa katika Dameski kwa jina la Yesu. Naye akawa pamoja nao katika Yerusalemu akiingia na kutoka.”

Maumivu ya kuvunjika kwa uhusiano.

Yohana 6:66 “Kwa ajili ya hayo wengi miongoni mwa wanafunzi wake wakarejea nyuma, wasiandamane naye tena.”

Hata hivyo Pamoja na kuwa Mungu huwaleta watu karibu nasi kama tulivyojifunza kutoka kwa Bwana Yesu ni jambo la kusikitisha kuwa, kuna wakati  mwingine wengine wataondoka kama ilivyokuwa tu kwa Yesu, watu au wanafunzi wengi siku hiyo waliamua kuondoka tena biblia inasema wasiambatane naye tena, hapa ni kwa sababu walishindwa kupokea mafundisho yake magumu katika akili zao, jambo hili linatufunza ya kuwa si kila mtu anayeanza safari pamoja nasi atakuwa pamoja nasi mpaka mwisho, na wakati huu ni wakati wa maumivu makali sana hakuna jambo linaumiza kama kuvunjika kwa mahusiano, yawe ya ndoa, yawe na ushirika, yawe ya kichungaji, kazini na kadhalika, lakini Mungu huruhusu watu hao waende na huo ndio unakuwa mwisho wa stori yao katika maisha yetu, inauma sana na inaumiza sana lakini hatuna budi kukubali, kama ilivyokuwa kwa Yesu Kristo ambapo wanafunzi wake walimuacha na hawakuambatana naye tena ndivyo ilivyo kwetu pia kuna kusudi kwa kila jambo katika maisha yetu,  wakati huo hakuna lolote tunaloweza kulifanya kuwafanya wabaki, Mungu tayari amekwisha kukusudia, wakuache wale wanaokupenda kwa dhati hawawezi kukuacha  watabaki na wewe iwe jua iwe mvua lakini wale ambao Mungu amekusudia waende wataenda tu hakua namna unaweza kulizuia hilo, hukuwaleta wewe kumbuka kwa hiyo  acha waende zao kwa amani, Kama Mungu ndiye aliyeamua waende hakuna unaloweza kulifanya wasiende?

Mungu ndiye mwenye funguo na mamlaka za kufunga na akifunga hakuna afunguaye, na akifungua hakuna anayeweza kufunga unaweza kujaribu kubembeleza na kujipendekeza kwa watu na ukajitahidi kuwapendeza na kufanya vizuri lakini kama Bwana hajaruhusu utakuwa unajisumbua bure, kile utakachokuwa unakitafuta ni kutafuta maumivu ya moyo tu, jaribu njia mpya na waache waende usiumie wala usikwazike ni Mungu ameruhusu, lazima tuamini kuwa Mungu ndiye anayedhibiti watu kuja na kuondoka katika maisha yetu na wengine huletwa kwetu kwa majira fulani tu kisha anawaondoa, unapoendelea kuwang’ang’ania watu ambao wamepoteza maana katika maisha yako maana yake unazuia kusonga kwako mbele au kukua katika kiwango kingine. Rafiki mimi ninajua uchungu wa kupoteza marafiki, ninapenda watu sana, sitaki kila ambaye amewahi kuwa rafiki yangu aniache, lakini uko wakati unalazimika kufanya hivyo, wako wapi uliosoma nao shule ya msingi, sekondari, vyuoni, na hata katika utumishi huu wako wapi? Wako wapi uliofanya nao kazi zamani,? Ulifika wakati waliondoka na Mungu aliwaficha na hukuweza kuwaona tena, kusudi la kuwepo kwao katika maisha yako lilikwisha kutimia na sasa Mungu anataka ufungue ukurasa mpya. Ona mfano wa maumivu yaliyomkuta Naomi:-

Ruthu 1:3-18 “Akafa Elimeleki, mumewe Naomi; na yule mwanamke akasalia na wanawe wawili. Nao wakaoa wake katika wanawake wa Moabu; na jina la mmoja aliitwa Orpa, na jina la wa pili Ruthu. Wakakaa huko yapata miaka kumi. Wakafa na Maloni na Kilioni wote wawili; na huyo mwanamke akawa amefiwa na wanawe wawili, na mumewe pia. Ndipo alipoondoka, yeye na wakweze, ili kurudi kutoka nchi ya Moabu; maana huko katika nchi ya Moabu amesikia ya kwamba Bwana amewajilia watu wake na kuwapa chakula. Basi akatoka pale alipokuwapo, na wakweze wawili pamoja naye; wakashika njia ili kurudi mpaka nchi ya Yuda. Kisha Naomi akawaambia wakweze wawili, Nendeni sasa mkarejee kila mmoja nyumbani kwa mamaye; Bwana na awatendee mema ninyi, kama ninyi mlivyowatendea mema hao waliofariki na mimi pia. Bwana na awajalie kuona raha kila mmoja nyumbani kwa mumewe. Kisha akawabusu; nao wakapaza sauti zao wakalia. Wakamwambia, La, sivyo; lakini tutarudi pamoja nawe kwa watu wako.Naye Naomi akasema, Enyi wanangu, mrejee; kwani kufuatana na mimi? Je! Mimi ninao watoto wa kiume tena tumboni mwangu, hata wawe waume zenu? Enyi wanangu, mrejee; nendeni zenu; kwa kuwa mimi ni mzee, siwezi kupata mume tena. Kama ningesema, Natumaini; kama ningepata mume hata usiku huu, na kuzaa watoto wa kiume; je! Mngesubiri hata watakapokuwa watu wazima? Mngejizuia msiwe na waume? La, sivyo, wanangu; maana ni vigumu kwangu kuliko kwenu, kwa sababu mkono wa Bwana umetoka juu yangu. Nao wakapaza sauti zao, wakalia tena, na Orpa akambusu mkwewe, lakini Ruthu akaambatana naye. Naye akasema, Tazama, shemeji yako amerejea kwa watu wake, na kwa mungu wake; basi urejee wewe umfuate shemeji yako. Naye Ruthu akasema, Usinisihi nikuache, Nirejee nisifuatane nawe; Maana wewe uendako nitakwenda, Na wewe ukaapo nitakaa. Watu wako watakuwa watu wangu, Na Mungu wako atakuwa Mungu wangu; Pale utakapokufa nitakufa nami, Na papo hapo nitazikwa; Bwana anitende vivyo na kuzidi, Ila kufa tu kutatutenga wewe nami. Basi alipomwona kuwa amekaza nia yake kufuatana naye, aliacha kusema naye.”

Tunasoma habari za Naomi, ambaye mumewe alifariki na kumuacha na watoto wawili ambao nao baadaye walioa, lakini vile vile walikufa katika nchi ya Moabu, kwa hiyo Naomi alibaki peke yake yeye na wakwe zake, Naomi aliamua kurudi kwao Yuda na aliwaeleza wakweze juu ya maamuzi yake mmoja aliitwa Orpa na mwingine Ruthu, Ruthu aliamua kubaki naye na Orpa aliamua kubaki katika inchi yake, wote walimpenda mkwe wao Naomi lakini Orpa aliamua kumbusu Naomi na kuondoka, Naomi hakuanza kulalamika kuwa Orpa anaondoka hata pamoja na wema wote aliomtendea na malezi yote aliyowapa Naomi alielewa kuwa huu ni msimu mpya ni msimu wa mabadiliko katika maisha kwa hiyo alikuwa na amani alipoachwa na Orpa alikubali kuwa Orpa aende na asiwe sehemu ya maisha yake tena, Mtu aliyekomaa kiroho/na kiufahamu huwaachia watu waende, unakubali Mungu awaondoe watu fulani katika maisha yako, Mungu ndiye anayefunga mlango au kufungua, lakini Ruthu aliamua kubaki na Naomi kwa gharama yoyote ile, hii ndio hali halisi, Yesu watu waliondoka na hakutikisika aliwauliza waliobaki naye je ninyi nanyi mwataka kuondoka? Aliendelea kuacha mlango wazi kwa kila anayetaka kumuacha, Naomi Orpa aliondoka ulikuwa wakati mgumu na wa maumivu makali sana, ulikuwa ni wakati mgumu ulikuwa ni wakati wa machozi lakini hakuna tunachoweza kufanya pale watu waliokuwa rafiki, waliokuwa ndugu waliokuwa jamaa zetu, waliokuwa wenzetu waliokuwa tunashinda nao, na kuzungumza nao wanapoamua kutuacha ni vema kukubali waende, Naomi alimbusu Orpa na kumuacha aende, kumbuka  hatuhitaji kufukuza mtu au kumaliza nao vibaya wala kuwa na uadui nao lakini sasa wanaondoka utafanya nini tuwaache waende zao kwa Amani huo ndio ukomavu wa kifikra na ukomavu kiroho na ujuzi, sio wewe tu utaacha wewe pia unaweza kuachwa na watu uliowapenda lakini wakawa hawakuhitaji tena huwezi kubadili pai isiwe 22/7  ni lazima ukubaliane na ukweli wa mambo hata kama ni mchungu kiasi gani waache waende! 

Yesu aliwahi kuwafundisha wanafunzi wake kuwa sio kila mahali watawakubali, ziko sehemu nyingine watu watakukataa hawatafungua mioyo yao kwako, watakukataa hawatakukaribisha unajua unachotakiwa kukifanya ni kukung’uta mavumbi ya miguu yako kisha enenda kule ambako watakukaribisha, hii sio kwa ugomvi ni sehemu ya kawaida kabisa katika maisha kwamba watu watakuja kwetu na kisha wataondoka na sisi halikadhalika.

Mathayo 10:13-14 “Na nyumba ile ikistahili, amani yenu na iifikilie; la, kwamba haistahili, amani yenu na iwarudie ninyi.Na mtu asipowakaribisha wala kuyasikiliza maneno yenu, mtokapo katika nyumba ile, au mji ule, kung'uteni mavumbi ya miguuni mwenu.”

Matendo 18:6-8 “Walipopingamana naye na kumtukana Mungu, akakung'uta mavazi yake, akawaambia, Damu yenu na iwe juu ya vichwa vyenu; mimi ni safi; tangu sasa nitakwenda kwa watu wa Mataifa. Akaondoka huko akaingia katika nyumba ya mtu mmoja jina lake Tito Yusto, mcha Mungu, ambaye nyumba yake ilikuwa mpaka mmoja na sinagogi. Na Krispo, mkuu wa sinagogi, akamwamini Bwana pamoja na nyumba yake yote. Wakorintho wengi waliposikia, waliamini, wakabatizwa.”

Usijisumbue na watu ambao hawakutaki, watu ambao hawaoni thamani yako, wala usijaribu kuwashawishi, endapo utafanya hivyo utajichelewesha na utajipatia fadhaa bure, Ni kweli Mungu anaweza kuwabadilisha  kama watatakiwa kukuunga mkono lakini kamwe usijaribu kujilazimisha kuungana na watu wasiotambua uthamani wako, damu ya kifalme ya Yesu Kristo inatitiririka katika mwili wako wewe sio wa kawaida wewe ni mali ya Mungu na ndio maana Mungu alikuokoa na amekuumba kwa sura na mfano wake kwa hiyo usiwashawishi watu wakukubali kama mioyo yao imefungwa, Mungu ameandaa watu tayari wanaotambua uthamani wako, inaweza kuwa inauma sana lakini ndio ukubwa achana nao waache waende, katika maisha yetu wako Orpa wengi lakini vile vile wako Ruthu wengi ambao wamepangiwa kutokutuacha watakaokaa nasi, na kuambatana nasi wanaoondoka ni kuwa Mungu amemalizana nao katika kusudi lao kwako na wanaobaki ni wale ambao Mungu anataka ushirikiane nao Baraka zako, wale walio kama Ruthu watabaki kuwa waaminifu kwako  na hawatakuacha daima, hatupaswi kumfukuza mtu wala kumpiga teke mtu lakini acha wao watupige teke na kutufukuza na hapo neema ya Mungu ya urafiki wetu kwao itakuwa imefikia ukingoni  inasikitisha inaumiza sana lakini huu ndio ukweli katika maisha.

Matendo 15:36-40 “Baada ya siku kadha wa kadha Paulo akamwambia Barnaba, Haya! Mrejee sasa tukawaangalie hao ndugu katika kila mji tulipolihubiri neno la Bwana, wa hali gani.Barnaba akaazimu kumchukua Yohana aliyeitwa Marko pamoja nao. Bali Paulo hakuona vema kumchukua huyo aliyewaacha huko Pamfilia, asiende nao kazini. Basi palitokea mashindano baina yao hata wakatengana. Barnaba akamchukua Marko akatweka kwenda Kipro.Lakini Paulo akamchagua Sila, akaondoka, akiombewa na wale ndugu apewe neema ya Bwana.”

Paulo na Barnaba walikuwa marafiki, waliitwa pamoja  na Roho Mtakatifu katika kazi ya huduma, waliihubiri injili kwa pamoja kimsingi Barnaba alikuwa ni kama Mchungaji wa Paulo mtume, ni yeye ndiye aliyemtambulisha kwa mitume na ni yeye aliye mpeleka Antiokia, walizoeana sana, waliitwa kwa pamoja na Roho Mtakatifu kwa kazi ya umisheni, lakini ulifika wakati wakaachana haikuwa kwa lengo baya wala kwa ugomvi, lakini ulifika wakati ambapo Mungu alikusudia kila mmoja awe na njia yake hili ni jambo la kawaida sana katika maisha wao tofauti yao ilikuwa ni Marko, nadhani inawezekana Marko alijisikia vibaya maana Paulo alimuona ni mtu dhaifu, Lakini Barnaba aliona Marko anahitaji malezi tu kwa hiyo kulitokea tofauti na kulitokea matengano, Lakini Mungu ni mmoja, miaka mingi baadaye, Paulo aliutambua umuhimu wa Marko na aliomba aungane naye maana anamfaa kwa huduma! Angalia:-

2Timotheo 4:10-11 “Maana Dema aliniacha, akiupenda ulimwengu huu wa sasa, akasafiri kwenda Thesalonike; Kreske amekwenda Galatia; Tito amekwenda Dalmatia. Luka peke yake yupo hapa pamoja nami. Umtwae Marko, umlete pamoja nawe, maana anifaa kwa utumishi.”

Paulo alimkumbuka Marko na kuagiza aletwe kwake kwa sababu ana faida nyingi sana kwa utumishi, kumbe kuna mtu anaweza asiwe na faida kwako leo, lakini akawa na faida kwako kesho, unaweza usimuhitaji mtu leo lakini ukamuhitaji mtu huyo kesho, Mungu ndiye anayehusika anaweza mtu asikufae kwa jua akakufaa kwa mfua na anaweza mtu asikufae kwa mvua akakufaa kwa jua hii ndio dunia ya Mola kwa hiyo tuheshimu mahuisiano sana  na kuyatunza isipokuwa pale to Mungu anapoamua huyu aende kule na huyu aje hapa kwa makusudi yake mema.

Wakati mwingine mafanikio yetu yanaweza kuwavuta watu wengi sana kwetu, na mapito yetu yanaweza kuwafanya wengi watukimbie, unapitia upweke? Wakati wa changamoto hakuna mtu wa kukutia moyo? Hii ilimpata Ayubu Maandiko yanasema watu wa nyumbani mwake walikuwa wengi sana ona

Ayubu 1:3 “Mali yake nayo yalikuwa ni kondoo elfu saba, na ngamia elfu tatu, na jozi za ng'ombe mia tano, na punda wake mia tano, NA WATU WA NYUMBANI WENGI SANA; basi hivi mtu huyo alikuwa ni mkuu sana kuliko watu wote wa upande wa mashariki.”

Unaona tunasoma kuwa watu wa nyumbani kwa Ayubu walikuwa wengi sana wakati wa mafanikio yake, lakini wakati wa dhiki yake watu wote walimuacha na kundoka zao, hata hivyo wakati wa mafanikio yake walirejea tena kwa wingi sana, hili nalo ni jambo la kawaida katika uanadamu kwa hiyo usivunjike moyo unapopitia upweke!  

Ayubu   42:10-12 “Kisha Bwana akaugeuza uteka wa Ayubu, hapo alipowaombea rafiki zake; Bwana naye akampa Ayubu mara mbili kuliko hayo aliyokuwa nayo kwanza. Ndipo wakamwendea nduguze wote, waume kwa wake, nao wote waliojuana naye hapo zamani, wakala chakula pamoja naye katika nyumba yake; nao wakamlilia na kumtuza moyo katika habari za huo uovu wote Bwana aliouleta juu yake; kila mtu akampa kipande cha fedha, na pete ya dhahabu kila mmoja. Basi hivyo Bwana akaubarikia huo mwisho wa Ayubu zaidi ya mwanzo wake; naye alikuwa na kondoo kumi na nne elfu, na ngamia elfu sita, na jozi za ng'ombe elfu, na punda wake elfu.”

Wakati mwingine watu, na marafiki zako watakuacha kwa sababu tu unapita katika hali ngumu, lakini wanaweza kukurudia tena hali inapokuwa nzuri hili nayo ni jambo la kawaida katika maisha na hatuna budi kulielewa na kukubaliana nalo. Jambo kubwa la msingi ni kwamba mahusiano yanapaswa kutunzwa na kuwa na Amani na watu woe ni swala la smingi sana tuwapo duniani. lakini watu wanapoondolewa kwetu, tumshukuru Mungu kwaajili yao                                  

Je ninyi nanyi mwataka kuondoka?

Yohana 6:67-69 “Basi Yesu akawaambia wale Thenashara, Je! Ninyi nanyi mwataka kuondoka? Basi Simoni Petro akamjibu, Bwana! Twende kwa nani? Wewe unayo maneno ya uzima wa milele Nasi tumesadiki, tena tumejua, ya kuwa wewe ndiwe Mtakatifu wa Mungu.”

Yesu anatufundisha kuwa yeye alikuwa tayari kuwaacha watu waende zao, Kama wamechagua kwenda hakuwalazimisha kubaki nao lakini aliwapa uhuru wa kuondoka ili wafanye maamuzi yao wenyewe, waache waende zao kwa Amani, kama wamejisikia raha kuwa mbali na wewe wamejisikia Amani kukuacha acha waende! Na kama wamejisikia kubaki acha wabaki na wewe usiwalazimishe, kulazimisha watu wawe nawe wakati hawana Amani ya kuwa na wewe kutasababisha uchungu katika maisha yako, kukosa utulivu na majuto, lakini kama utawaacha waende watapata nafasi mpya na kujiamulia mambo yao wenyewe, wape watu uhuru wa kuamua  na Amani ya Mungu itaamua. Na huu ndio ukomavu wa kiroho, kiufahamu na kihekima. Let them go !

Wafilipi 4:6-7 “Msijisumbue kwa neno lo lote; bali katika kila neno kwa kusali na kuomba, pamoja na kushukuru, haja zenu na zijulikane na Mungu. Na amani ya Mungu, ipitayo akili zote, itawahifadhi mioyo yenu na nia zenu katika Kristo Yesu.”

Amini katika kusudi la Mungu kwamba Mungu anaporuhusu watu waende zao na au wabaki na wewe ufahamu kuwa Mungu ana mpango mkubwa na mpya na kila mmoja, inaweza kuwa ngumu kuelewa lakini hatuna budi kuamini katika mpango wa Mungu kwa kuwa Mungu ni mwema, watu wanapoondoka katika maisha yako iwe kwa wema au kwa ubaya bado fahamu ya kuwa Mungu ana mpango mwema kwenu wote yeye huweza kuitumia njia yoyote ile katika kutokeza jambo lililo jema zaidi.

Warumi 8:28 “Nasi twajua ya kuwa katika mambo yote Mungu hufanya kazi pamoja na wale wampendao katika kuwapatia mema, yaani, wale walioitwa kwa kusudi lake.”              

Rafiki wa kweli ni yule atakayesimama na wewe hata katika hali ngumu, Petro na wale thenashara walichagua kubaki na Yesu, Petro alisema tuende wapi Bwana wewe una maneno ya uzima wa milele, wako marafiki watakaa na wewe kwa muda mfupi, au watajitokeza kwako katika wakati Fulani maalumu na kisha watakoma lakini marafiki kama Petro kwa Yesu Kristo watamaanisha kubaki na wewe, kwa hiyo ni Muhimu kutambua umuhimu wao na kumshukuru Mungu kwaajili yao. Wakati wote kumbuka kuwa uhusiano wowote ule uwe wa muda au ule wa kudumu una kitu cha kutufundisha katika maisha yetu, hatukutanishwi na watu kwa bahati mbaya, Mungu hakumuumba mwanadamu awe peke yake, tunahitajiana, Lakini Mungu huruhusu watu waje na kuondoka katika maisha yetu kwa kusudi maalumu,  jambo kubwa na la msingi ni sisi kuendelea kuwa waaminifu katika kila aina ya uhusiano ambao Mungu ametupa kumbuka mahusiano yanapovunjika inaleta maumivu makali sana lakini wale wanaoondoka waache waende na wale wanaobaki kaa nao kumbuka kuwa ni Mungu ndiye anayewashika mkono na kuwaleta kwetu kwa hiyo amini katika mchakato huo na utakubali ukweli huu mchungu katika maisha, wafurahie sana wale wote ambao Mungu anawaleta katika maisha yako ukijua kuwa ni sehemu ya mpango wa Mungu,  wakubali wale wote ambao Mungu ameruhusu waende zao mbali na wewe ukijua pia kuwa Mungu ana mpango mwema, thamini umuhimu na msingi wa marafiki  hususani wale wanaobaki kuwa waaminifu kwako hasa wakati wa majaribu na wakati wa mambo magumu, waheshimu wote wapende wakubali lakini usilazimishe mtu akupende au awe na wewe hii haimaanishi uwatendee watu kikatili hapana lakini jifunze kuwa kama Yesu, Yesu aliwahoji hata wale waliobaki je ninyi nanyi mwataka kuondoka?  

Hatima yako haiko mikononi mwa waliokuacha, wala Mungu haitaji lolote uliloliacha au chochote ulichopoteza kupitia marafiki walioondoka, jambo kubwa la msingi uwe na Amani lakini usilazimishe watu wakupende na kukubali au wakuamini, ukiona wamekuacha maana yake huwahitaji tena, wao sio sehemu ya mpango wa Mungu katika maisha yako tena na Mungu ana mpango mwema na wewe na hata wale wanaokusema vibaya waache waseme, mimi nimewahi kusikia habari za mtu anayenisema vibaya na nikaonyeshwa sijawahi kumkataza wala kumbeleza aniseme vizuri, ninajua tu kuwa Mungu ameruhusu wawepo watu watakaonisema vizuri na wawepo watu watakaonisema vibaya wote wana faida katika mapenzi ya Mungu, wanaonisema vibaya wananisaidia nisiwe na kiburi, nikumbuke kuwa mimi ni mwanadamu na nizidi kunyenyekea na wale wanaofaidika na huduma yangu watamshukuru Mungu kwaajili yangu, sina muda wa kumbembeleza mtu asiniseme vibaya, siumii tena na wanaosema vibaya wala siwezi kutukuka watu wakinisifu, ninanyenyekea kwa Mungu kwa sababu mimi ni udongo tu, sikuja duniani kusifiwa, nimekuja duniani kutimiza kile ambacho Mungu amekikusudia katika maisha yangu na hivyo kile nitapangiwa na Mungu kukifanya nitakifanya, Petro alitambua ya kuwa Yesu ana maneno ya uzima wa milele, na ya kuwa ni Mtakatifu wa Mungu yaani ni Masihi.

Bwana ampe neema kila moja wetu kuelewa makusudi ya somo hili kwa kina na mapana na marefu katika jina la Yesu Amen!

 

Na. Rev Innocent Samuel Kamote

Mkuu wa wajenzi mwenye Hekima!


Alhamisi, 10 Oktoba 2024

Uwaheshimu wajane walio wajane kweli kweli!


1Timotheo 5:1-5 “Mzee usimkemee, bali umwonye kama baba; na vijana kama ndugu; wanawake wazee kama mama; wanawake vijana kama ndugu wa kike; katika usafi wote. Uwaheshimu wajane walio wajane kweli kweli. Lakini mjane akiwa ana watoto au wajukuu, na wajifunze kwanza kuyatenda yaliyo wajibu wao kwa jamaa zao wenyewe, na kuwalipa wazazi wao. Kwa kuwa hili lakubalika mbele za Mungu. Basi yeye aliye mjane kweli kweli, ameachwa peke yake, huyo amemwekea Mungu tumaini lake, naye hudumu katika maombi na sala mchana na usiku.”




Utangulizi:


Moja ya maswala ambayo nyakati za kanisa la kwanza yalipewa kipaumbele sana ni pamoja na kuwahudumia wanawake waliokuwa wajane kwelikweli, Swala zima la kuwakumbuka wajane lilipewa uzito mkubwa sana katika kanisa la kwanza kuliko ilivyo katika nyakati za leo, na inawezekana moja ya sababu kubwa inayofanya kanisa la leo kujisahau ni pamoja na kutokuwa na ufahamu wa kutosha kuhusu somo hili, Lakini kwa neema ya Mungu, Roho Mtakatifu Mwalimu mkuu leo anataka kutukumbusha tena namna na jinsi ya kuwaheshimu wajane kama tutakavyoweza kujifunza kwa kina na mapana na marefu katika siku hii ya leo.


Yakobo 1:25-27 “Lakini aliyeitazama sheria kamilifu iliyo ya uhuru, na kukaa humo, asiwe msikiaji msahaulifu, bali mtendaji wa kazi, huyo atakuwa heri katika kutenda kwake. Mtu akidhani ya kuwa anayo dini, wala hauzuii ulimi wake kwa hatamu, hali akijidanganya moyo wake, dini yake mtu huyo haifai.Dini iliyo safi, isiyo na taka mbele za Mungu Baba ni hii, Kwenda kuwatazama yatima na wajane katika dhiki yao, na kujilinda na dunia pasipo mawaa.” 


Mungu anawajali sana wajane na kujihusisha sana na maisha yao na anatoa wito kwa kanisa lake na watu wake na jamii kufanya kitu kwaajili ya Wajane, Mungu aliwapa wajane kipaumbele kikubwa sana nyakati za agano la kale na kuwaweka katika uangalizi maalumu chini yake mwenyewe. 


Zaburi 68:4-6 “Mwimbieni Mungu, lisifuni jina lake, Mtengenezeeni njia ya barabara, Apitaye majangwani kama mpanda farasi; Jina lake ni YAHU; shangilieni mbele zake. Baba wa yatima na mwamuzi wa wajane, Mungu katika kao lake takatifu. Mungu huwakalisha wapweke nyumbani; Huwatoa wafungwa wakae hali ya kufanikiwa; Bali wakaidi hukaa katika nchi kavu.”

 

Kutokuwafikiria wajane nyakati za kale kulifikiriwa kuwa ni moja ya sababu ya kuleta maovu na changamoto katika maisha yako, na ndio maana unaweza kuona Yakobo akifikiri ya kuwa dini ya kweli ni lazima ihusishe kuwaangalia au kuwajali yatima na kuangalia mahitaji yao, Ayubu aliwahi kusema hivi alipokuwa akijitetea sababu ya changamoto zilizompata katika maisha yake na rafiki zake nay eye akadhani kuwa labda ni moja ya sababu ya mateso yake:-


Ayubu 31:15-17 “Je! Huyo aliyenifanya mimi ndani ya tumbo, siye aliyemfanya na yeye? Si yeye mmoja aliyetufinyanga tumboni? Ikiwa nimewanyima maskini haja zao, Au kama nimeyatia kiwi macho ya mwanamke mjane; Au kama nimekula tonge langu peke yangu, Mayatima wasipate kulila;”


Kwa hiyo ilieleweka wazi katika nyakati za waanzilishi wa Imani ya kuwa kutokuwajali yatima kunaleta mikosi na balaa kwa sababu kutokuwajali hao au kuwadhulumu na kutokuwapatia haki pamoja na yatima kunaweza kuwa sababu ya laana nyingi, na ndio maana utaweza kuona kuwa nyakati za kanisa la kwanza kulikuwepo na mgao maalumu wa mahitaji na chakula kwaajili ya wajane  na hali kadhalika utaweza kuona katika kifungu chetu cha msingi Paulo Mtume akimuagiza Timotheo kuwaheshimu wajane walio wajane kweli kweli.

Kumbukumbu 24:17-22 “Usipotoshe hukumu ya mgeni, wala ya yatima; wala usitwae mavazi ya mjane, yawe rehani; bali kumbuka ya kuwa ulikuwa mtumwa katika Misri, Bwana, Mungu wako, akakukomboa huko; kwa hiyo nakuamuru kutenda neno hili.Uvunapo mavuno yako katika shamba lako, ukasahau mganda shambani, usirudi kuuchukua; na uwe wa mgeni, au yatima, au mjane; ili Bwana, Mungu wako, akubariki katika kazi yote ya mikono yako. Utakapochuma matunda ya mizeituni yako, usirudi kuchuma mara ya pili; yaliyobaki apewe mgeni, na yatima, na mjane. Uchumapo zabibu katika shamba lako la mizabibu, usichume mara ya pili; zilizobaki apewe mgeni, na yatima, na mjane.Nawe kumbuka ya kuwa ulikuwa mtumwa katika nchi ya Misri; kwa hiyo nakuamuru kutenda neno hili.”


Kwa msingi huu leo tutachukua muda kujifunza sasa kwa kina na mapana na marefu namna na jinsi tunavyoweza kuwatambua na kuwatendea mema au kuwaheshimu wajane walio wajane kwelikweli na tutajifunza somo hili muhimu kwa kuzingatia vipengele vifuatavyo:-


Maana  ya neno Mjane 

Ufahamu kuhusu changamoto wanazokutana nazo wajane 

Uwaheshimu wajane walio wajane kweli kweli


Maana ya neno Mjane


Neno mjane ambalo katika kiingereza linajulikana kama neno “widow” katika biblia ya kiibrania linatumika neno  “almānāh”   na katika maandiko ya kiyunani linatumika neno “Chēra”  yote yakiwa na maana ya Mwanamke aliyepoteza mume wake kwa sababu ya kifo na ambaye hajaolewa tena, Mwanamke aliyeachwa baada ya kifo cha mumewe, Mwanamke aliyebaki peke yake, ni mwanamke ambaye mumewe amafariki na ameachwa mwenyewe na kwa sababu hiyo anakutana na changamoto kadhaa wa kadhaa katika jamii, ni mwanamke aliyefiwa lakini anakabiliwa na mapungufu, anakabiliwa na uhitaji, hana ulinzi wala msaidizi, hana hali nzuri ya kiuchumi na kihisia anapitia mambo magumu. Kutokana na hali hiyo nyakati za agano la kale wajane waliwekwa katika kundi la watu wanaohitaji msaada kama wakimbizi, masikini na yatima, au pamoja na kundi la walawi, waliokuwa watumishi. 


Kumbukumbu 14:27-29 “na Mlawi aliye ndani ya malango yako usimwache, kwani hana fungu wala urithi pamoja nawe. Kila mwaka wa tatu, mwisho wake, toa fungu la kumi lote la maongeo yako ya mwaka huo, uliweke ndani ya malango yako; na Mlawi kwa kuwa hana fungu wala urithi pamoja nawe, na mgeni, na yatima, na mjane aliyefiliwa na mumewe, walio ndani ya malango yako, na waje wale na kushiba; ili kwamba Bwana, Mungu wako, akubarikie katika kazi yote ya mkono wako uifanyayo.”


Kuwajali wajane kama ilivyo kuwajali walawi, na yatima na wageni na masikini, katika maagizo ya Mungu kulikuwa kunafungua milango ya Baraka kubwa sana katika maisha ya wanadamu, maandiko yaaagiza kuwa watu hao waheshimiwe maana yake mtu asitumie nafasi ya ujane wao kuwadhulumu, kuwaonea na kuwafanyia jambo lolote lisilofaa, wakati mwingine katika hali ya ujane hivyo ziko mila na desturi mbaya miongni mwa jamii, na fikra potofu ambapo pia watu hao hufikiriwa kuwa wana nuksi, Mungu aliliona hilo na kulichungulia na anaweka katika utaratibu wa neno lake kuwa watu hao wapewe kipaumbele maalumu, aliwataka Israel hata wanapovuna chakula wabakize makombo ili yamkini watu hao duni wapate cha kuokoteza nyuma ya mashamba ya wenye uwezo. Pia Mungu aliweka sheria nyinginezo mbalimbali za kimila ili wajane warithiwe kwa kusudi la kuinua uzao wa Ndugu au kuwapa ulinzi na kadhalika hii yote ilikuwa ni kwa sababu ya kutafuta kuwatunza


Nyakati za kanisa la kwanza Mitume walikuwa na ufahamu kuhusu huduma kwa wajane na moja kwa moja tunaona nyakati za kanisa la kwanza kulikuwa na huduma maalumu ya chakula na mahitaji mengine na mgao wa kila siku kwaajili ya wajane 


Matendo 6:1-4 “Hata siku zile wanafunzi walipokuwa wakiongezeka hesabu yao, palikuwa na manung'uniko ya Wayahudi wa Kiyunani juu ya Waebrania kwa sababu wajane wao walisahauliwa katika huduma ya kila siku. Wale Thenashara wakawaita jamii ya wanafunzi, wakasema, Haipendezi sisi kuliacha neno la Mungu na kuhudumu mezani. Basi ndugu, chagueni watu saba miongoni mwenu, walioshuhudiwa kuwa wema, wenye kujawa na Roho, na hekima, ili tuwaweke juu ya jambo hili; na sisi tutadumu katika kuomba na kulihudumia lile Neno.”

 

Ufahamu kuhusu changamoto wanazokutana nazo wajane 


Kabla ya kujifunza kwa kina na mapana na marefu, kwanini Mungu anawapa kipaumbele Wajane, ni muhimu kukumbuka kuwa wajane ni watu wanaopitia changamoto kadhaa wa kadhaa ambazo inawezekana watu wengi wakawa hawafahamu na au labda tu hatujawahi kutoa kipaumbele lakini mara tu baada ya mjane kupoteza mwenzi wake aliyeishi naye kwa muda mrefu, jambo ambalo linamuacha akiwa mpweke na mwenye msongo wa mawazo, na msiba unapoisha tu mjane huanza kujihisi kuwa ametelekezwa, au ametupwa na hapo ndipo neno la Mungu linatuagiza kujali na kutambua mahitaji yao na kuwatia moyo kwa kuwabebea mizigo wa moyoni.


Changamoto za kihisia – wote tunatambua kuwa hakuna jambo baya duniani kama kufiwa, linapokuja swala la msiba wewe lisikie kwingineko tu lakini omba Mungu lisikukute, kufiwa ni jambo zito zito zito mno, na kufiwa na mtu aliye karibu na mliyeishi naye kwa muda mrefu kunaacha mshituko mkubwa, simanzi nzito, kupoteza, upweke, kuachwa na kutelekezwa, linapokukuta swala la msiba wa mtu ambaye alikuwa ni kipenzi chako wa karibu haijalishi kuwa mlikuwa mkifarakana au kugombana ghafla unahisi kama umeadhibiwa, umeumbuka, ni kama una nuksi au dunia na Mungu amekukataa, hisia hizo zote zinakuwa juu ya mjane hata kama atakuwa ameachiwa mali nyingi kiasi gani, lakini kibinadamu linakuwa ni jeraha la kimaisha. 


Kutelekezwa katika kiingereza linatumika neno abandonment  ambalo maana yake ni  leaving someone or ending or stopping something usually forever, kumuacha mtu, au kumtupa, au kumalizana naye au kumaliza uhusiano na yeye, au kuacha kuwasiliana naye na kwa kawaida milele, hili ni tukio baya sana ambalo kimsingi Mungu hawezi kuthubutu kulifanya. 


Maombolezo 3:3-33 “Kwa kuwa Bwana hatamtupa mtu Hata milele. Maana ajapomhuzunisha atamrehemu, Kwa kadiri ya wingi wa huruma zake. Maana moyo wake hapendi kuwatesa wanadamu. Wala kuwahuzunisha.” 


Kwa msingi huo inapotokea Mungu ameruhusu mwanadamu Fulani hasa mume kuondoka katika ulimwengu huu, mjane hupatwa na hisia za kutupwa, na hasa pale waombolezaji wanapoondoka na mfiwa anaanza kubaki mwenyewe, uhalisia wa msiba ndio unaanza, mfiwa anajikuta anajuta, anaanza kuhisi umuhimu wa yule aliyeonmdoka, pengo lake, na kama aliugua unaanza kuhisi kuwa labda ungempeleka hospitali Fulani ingekuwa kuna nafuu na kadhalika kwa hiyo simanzi huanza kuusonga moyo wa mjane. Kwa hiyo mara moja mwanamke anapofiwa na Mumewe watu wa Mungu hawana budi kujifunza namna ya kuwatetea wajane na kuwalinda jambo hili litawaletea Baraka kubwa sana


Isaya 1:16-17 “Jiosheni, jitakaseni; ondoeni uovu wa matendo yenu usiwe mbele za macho yangu; acheni kutenda mabaya; jifunzeni kutenda mema; takeni hukumu na haki; wasaidieni walioonewa; mpatieni yatima haki yake; mteteeni mjane.


Zekaria 7:9-10 “Bwana wa majeshi amesema hivi, ya kwamba, Fanyeni hukumu za kweli, kila mtu na amwonee ndugu yake rehema na huruma; tena msimdhulumu mjane, wala yatima, wala mgeni, wala maskini; wala mtu awaye yote miongoni mwenu asiwaze mabaya juu ya ndugu yake moyoni mwake.” 


Changamoto za kiuchumi -  Nyakati za Biblia kwa kiwango kikubwa sana au zamani wanawake wengi walikuwa wanawategema waume zao katika maswala ya kiuchumi, hata siku za leo pamoja na kuwa wanawake wengi wamepata mwamko mkubwa sana wa kujishughulisha hata hivyo bado ni jukumu la Mume kuitunza familia na kuitia moyo, kuisimamia kama kichwa cha nyumba na kama wanasaidiana ni njema sana sasa inapotokea mume amefariki bado inaleta mtikisiko mkubwa wa kiuchumi kwa mmoja anayesalia kwaajili ya kuitunza familia iliyobaki naye kwa hiyo changamoto za kiuchumi ni moja ya tatizo linalowakumba wajane, wanaweza kupoteza njia na namna ya kujikimu, na kwa sababu ni wanawake wakati mwingine hata kimila na desturi za baadhi ya watu wanaweza kuwaonea  na hata kutaka kuwadhulumu wanawake hao wajane  na ndio maana utaweza kuona Mungu aliweka sheria kali sana za kuwalinda wajane, kwani wakati mwingine pia walikabiliwa na madeni waliyoyaacha waume zao, au kupokonywa rasilimali na kadhalika  


Kutoka 22:22-24 “Usimtese mjane ye yote aliyefiwa na mumewe, wala mtoto yatima. Ukiwatesa watu hao katika neno lo lote, nao wakanililia mimi, hakika yangu nitasikia kilio chao, na hasira yangu itawaka moto, nami nitawaua ninyi kwa upanga; na wake wenu watakuwa wajane, na watoto wenu mayatima.


2Wafalme 4:1-7 “Basi, mwanamke mmoja miongoni mwa wake za wana wa manabii alimlilia Elisha, akasema, Mtumishi wako mume wangu amekufa; nawe unajua ya kuwa mtumishi wako alikuwa mcha Bwana; na aliyemwia amekuja ili ajitwalie wana wangu wawili kuwa watumwa.Elisha akamwambia, Nikufanyie nini? Niambie; una kitu gani nyumbani? Akasema, Mimi mjakazi wako sina kitu nyumbani, ila chupa ya mafuta. Akasema, Nenda, ukatake vyombo huko nje kwa jirani zako wote, vyombo vitupu; wala usitake vichache. Kisha uingie ndani, ukajifungie mlango wewe na wanao, ukavimiminie mafuta vyombo vile vyote; navyo vilivyojaa ukavitenge. Basi akamwacha, akajifungia mlango yeye na wanawe; hao wakamletea vile vyombo, na yeye akamimina. Ikawa, vilipokwisha kujaa vile vyombo, akamwambia mwanawe,Niletee tena chombo. Akamwambia, Hakuna tena chombo. Mafuta yakakoma. Ndipo akaja akamwambia yule mtu wa Mungu. Naye akasema, Enenda ukayauze mafuta haya, uilipe deni yako; nayo yaliyosalia uyatumie wewe na watoto wako.” 


Aidha Mungu aliagiza kuhakikisha kuwa unawasaidia wajane kwa masazo ya chakula hasa wakati wa mavuno ili na wao waweze kuokoteza na kukidhi mahitaji yao, kwa lugha nyingine Mungu anataka tuwakarimu wajane, tusiende kwao mikono mitupu, tuwasaidie tuwabebe kiuchumi, lakini tuwakumbuke katika maisha


Kumbukumbu 24:19-21 “Uvunapo mavuno yako katika shamba lako, ukasahau mganda shambani, usirudi kuuchukua; na uwe wa mgeni, au yatima, au mjane; ili Bwana, Mungu wako, akubariki katika kazi yote ya mikono yako. Utakapochuma matunda ya mizeituni yako, usirudi kuchuma mara ya pili; yaliyobaki apewe mgeni, na yatima, na mjane. Uchumapo zabibu katika shamba lako la mizabibu, usichume mara ya pili; zilizobaki apewe mgeni, na yatima, na mjane.


Changamoto za upweke – Wajane katika namna mbalimbali huwa wanahisi kukumbwa na upweke, kuondokewa na ulinzi na heshima, wanahisi wametengwa na jamii kwa kiwango kikubwa, mabadiliko makubwa na ya ghafla katika hali ya ndoa yanaingiwa na giza,  na wakati mwingine katika jamii nyingine hufikiriwa kuwa ni mojawapo ya sababu ya vifo vya waume zao, na hivyo hulaumiwa  jambo hili na sababu nyinginezo zinaweza kuchangia wao kuhisi kutengwa na jamii, kuwa wapweke, na kutoa mwanya mdogo sana kati ya changamoto za kihisia na upweke na kuongeza madonda mwilini, wanawake wengine hufikiriwa kuwa na nuksi au kusababisha balaa na wakati mwingine wanaume wengine hufikiri kuwa mwanamke huyu ana nuksi na husababisha vifo vya wanaume wengine. 


Mwanzo 38:6-11 “Yuda akamwoza mke Eri, mzaliwa wake wa kwanza, na jina lake huyo mke ni Tamari. Naye Eri, mzaliwa wa kwanza wa Yuda, alikuwa mbaya machoni pa BWANA; na BWANA akamwua. Yuda akamwambia Onani, Uingie kwa mke wa nduguyo, ukamwoe, ukamwinulie nduguyo uzao. Onani alijua ya kwamba huo uzao hautakuwa wake, ikawa, alipoingia kwa mke wa nduguye, akamwagia chini asimpe nduguye uzao. Neno hili alilolifanya likawa baya machoni pa BWANA, basi akamwua yeye naye. Yuda akamwambia Tamari mkwewe, Ukae mjane nyumbani mwa baba yako hata Shela mwanangu atakapokuwa mtu mzima, maana alisema, Asipate kufa yeye kama nduguze. Basi Tamari akaenda, akakaa nyumbani mwa babaye.” 


Tamari alikuwa moja ya wahanga wa ujane, alifiwa na waume wawili na Yuda aliahidi kumuoza mwanae mwingine aitwaye Shela, hata hivyo hakufanya hivyo kwa hofu kuwa mwanamke huyu ana nuksi huenda atasababisha kifo cha mwanaye mdogo, kwa hiyo Tamari alijilipizia kisasi kwa kulala na Yuda mwenyewe na ndipo ukoo wa Masihi ulipotokea kwa kumzaa Peresi Zera kupitia Yuda mwenyewe badala ya watoto wake, ujane una mitihani mingi, wako wanaolenga mali zao, wako wanaowafikiria kuwa labda ni wagonjwa na wanawaogopa hata kuwaoa wakijiuliza waume zao wamekufaje, wako wanaowamendea wawatweze, na wako wanaowatamani kuwatumia tu kimwili kutokana na kujua upweke walionao 


Changamoto za kimalezi – Moja ya kazi ngumu sana kwa kina mama wajane ni malezi ya watoto, wote tunafahamu changamoto za kuwa mlezi peke yako, sauti ya mume ni sauti ya mamlaka ina nguvu katika makemeo ya watoto, haijalishi nani huwa ni mkali katika malezi lakini watoto hukaa vizuri sana wanapolelewa na pande zote mbili za wazazi, kwa hiyo kama wako watoto na mume amefariki mjane huwa na wakati mgumu sana wa kuwa mlezi pekee, kukabiliana na malimwengu inaweza kuwa rahisi kuliko kulea watoto peke yako  bila mwenzi wako,  watoto watahisi lile pengo ambalo baba yao angeweza kutosha,  yako mambo ambayo baba anaweza kuwa alikuwa mzuri katika hilo kwa hiyo mama atatakiwa kufanya mara dufu kuweza kuziba, hofu kubwa ikiwa kila mtoto atajihisi sasa ni kiongozi kwa nafsi yake na hivyo mwanamke huyu atabaki anapambana kuhakikisha kuwa kila kitu kina kaa mahali pake. Ni kwaajili ya haya Mungu mwenyewe alibeba jukumu la kuwa baba wa yatima na mwamuzi wa wajane. 


Zaburi 68:4-6. “Mwimbieni Mungu, lisifuni jina lake, Mtengenezeeni njia ya barabara, Apitaye majangwani kama mpanda farasi; Jina lake ni YAHU; shangilieni mbele zake. Baba wa yatima na mwamuzi wa wajane, Mungu katika kao lake takatifu. Mungu huwakalisha wapweke nyumbani; Huwatoa wafungwa wakae hali ya kufanikiwa; Bali wakaidi hukaa katika nchi kavu


Changamoto za kiroho – hali ya kupoteza mume huhesabika kama adhabu kubwa sana kwa mwanamke kwa hiyo wengi hugeuka kuwa wakali sana wakitetea maslahi yao na kwa Mungu wanakuwa na mgogoro naye, wanahisi Mungu amewaacha na kuwatelekeza hii ni fikira ya kawaida kwa wajane wengi na ndio maana Mungu akajiwahi katika maandiko kusimama kama mtetezi wao, wengi huwa na maswali mazito hata wakati wa Msiba huwa  wanalia huku wakimuuliza Mungu kwanini kwanini, huwa wanahoji kwanini Mungu achukue mume wake, kwa nini maisha yawe hivi au vile baada ya wao kupoteza mume?  Wanahisi kuwa maisha hayana maana na kupata maluwe luwe ya kiroho wengi huchanganyikiwa na kutokuwa sawasawa, ni ukweli ulio wazi kuwa wanapatwa na mshituko wa kiroho na kuwa katika wimbi kubwa la msongo wa mawazo, msongo wa mawazo wa mtu aliyefiwa na mume ni mara nne ya wale wenye ndoa yenye mgogoro, kama alimuombea sana mumewe amuokoe na mauti na bado akafa, mjane anaweza kumuona Mungu kuwa hana maana kabisa  na kama asipojengwa vema kiroho anaweza kupoteza uwepo wa Mungu nahata kuvamiwa na pepo kwa sababau ya kuelemewa na huzuni na vita ya kiroho. Wakati mwingine wajane hufikiri kuwa Mungu anawakumbusha dhambi zao walizozifanya zamani pale wanapopata majaribu mengine ili hali wao ni wajane


1Wafalme 17:17-22 “Ikawa, baada ya hayo, mwana wake yule mwanamke, bibi wa nyumba ile, akaugua; ugonjwa wake ukazidi hata akawa hana pumzi tena. Akamwambia Eliya, Nina nini nawe, Ee mtu wa Mungu? Je! Umenijia ili dhambi yangu ikumbukwe, ukamwue mwanangu? Akamwambia, Nipe mwanao. Akamtoa katika kifua chake, akamchukua juu chumbani mle alimokaa mwenyewe, akamlaza kitandani pake. Akamwomba Bwana, akanena, Ee Bwana, Mungu wangu, je! Umemtenda mabaya mjane huyu ninayekaa kwake hata kumfisha mwanawe. Akajinyosha juu ya mtoto mara tatu, akamwomba Bwana, akanena, Ee Bwana, Mungu wangu, nakusihi, roho ya mtoto huyu imrudie ndani yake tena. Bwana akaisikia sauti ya Eliya; na roho ya mtoto ikamrudia, akafufuka.


Changamoto za kisaikolojia – Ni ukweli usiopingika ya kuwa wanawake wajane wanapitia changamoto nyingi sana za kisaikolojia, tafiti zinaonyesha hivyo japo kanisa linaweza lisiwe na utafiti wa kina au likawa linapuuzia hilo, lakini mgandamizo wa mawazo, mashaka, hofu  na ugumu wa maisha na kukosa tendo la ngono kunatengeneza changamoto kubwa na nyingi za kisaikolojia, wajane watateseka kijamii, kiutamaduni, kiimani,kimila, kiuchumi, kiroho na kisheria  na huku upande mwingine wakiwa hawana mume  wanayapitia haya kimya kimya wakati mwingine jamii ikiwa haina hata taarifa, wanakutana na unyanyasaji wa kisaikolojia wa aina mbalimbali licha ya maneno wanayokutana nayo, ukweli ni kuwa sio rahisi sana kujua wajane wanapitia changamoto gani mpaka uwe makini, hatuwezi kushughulikia kila kitu wanachopitia lakini angalau tunaweza kuwapunguzia.  Katika moja ya utafiti uliofanyika nchini kenya katika kaunti ya Kisumu wanawake 50 walifanyiwa utafiti wa kisayansi na kujulikana kuwa bila kujali kuwa waume zao walifariki katika namna ipi  wanawake hao waligundulika kuwa na changamoto ya fadhaa kubwa, kukosa msaada, maumivu makali ya ndani, maombolezo yasiyokoma, hofu na woga, utafiti huo uliotumia njia mchanganyiko za maswali,  na kuwahoji uso kwa uso, ukusanyaji wa taarifa  na tafiti za kiushauri tafiti hizo zilizofanywa na Atindabilal, Bamford, Adatara, Nauko na Obenwa mwaka wa 2014  ulibaini kuwa changamoto wanazokutana nazo wajane kisaikolojia na kuzinukuu kama walivyoorodhesha kwa kiingereza “mental and emotional challenges such as grief, loneliness, isolation, anxiety, low self – esteem, denial, withdraw, sexual unfulfillment and depressed moody, kwa tafasiri yangu wanapata changamoto za kiakili, kihisia, kumezwa na huzuni, upweke, kutengwa, kujitenga, wasiwasi, kutokujithamini, kujikataa, kukosa ngono, na hisia zenye msongo  kwa msingi huu kama matabibu wa kisaikolojia wanaweza kufanya utafiti huu na kugundua changamoto wanazozipitia wajane ukweli ni kuwa viongozi wa kiroho hususani watumishi wa Mungu wachungaji wanapaswa kujua pamoja na kanisa kuwa ujane sio tatizo dogo, na ndio maana nyakati za kanisa la kwanza lakini pia Mungu menyewe tumeona akijihusisha kutatua changamoto za wajane, dunia inakisiwa kuwa na wajane wapatao milioni 245 na kati ya hao wanaoishi kwenye umasikini wa kutupwa ni milioni 115 wengine wakiteseka kimila kama huko Nigeria ambako wengine huvamiwa na ndugu wa mume na wanachukua kila kilicho cha ndugu yao na kuwaacha wajane katika mazingira magumu sana kwahiyo unaweza kupata picha kuwa changamoto hii ni kubwa kwa kiasi gani, kwa hiyo kanisa haliwezi kukaa kimya na kuacha kuwa na huduma au kitengo na namna ya kuwahifadhi wajane sawa tu na mtazamo wa nyakati za kanisa la kwanza ulivyokua, tunaweza tusitimize mahitaji yao yote lakini tunaweza kuwapunguzia changamoto zao ili wasiwe na msiba juu ya msiba, Yesu alipunguza maumivu ya mwanamke mjane katika lango la mji wa Naini ambaye licha ya kuwa alifiwa na mumewe sasa watu wa mji walikuwa wakienda kumzika na mwanae wa pekee, hii ilikuwa huzuni juu ya huzuni ashukuriwe Mungu mwenye kujali, Yesu alimpunguzia mwanamke huyu majonzi  


Luka 7:11-16. “Baadaye kidogo alikwenda mpaka mji mmoja uitwao Naini, na wanafunzi wake walifuatana naye pamoja na mkutano mkubwa. Na alipolikaribia lango la mji, hapo palikuwa na maiti anachukuliwa nje, ni mwana pekee wa mamaye ambaye ni mjane, na watu wa mjini wengi walikuwa pamoja naye. Bwana alipomwona alimwonea huruma, akamwambia, Usilie. Akakaribia, akaligusa jeneza; wale waliokuwa wakilichukua wakasimama. Akasema, Kijana, nakuambia, Inuka. Yule maiti akainuka, akaketi, akaanza kusema. Akampa mama yake. Hofu ikawashika wote, wakamtukuza Mungu, wakisema, Nabii mkuu ametokea kwetu; na, Mungu amewaangalia watu wake.”


Sisi kama kanisa sasa tunaweza kufanya nini kwaajili ya kushughulika na changamoto hizi wanazokutana nazo wajane hili sasa linatuleta katika sehemu muhimu ya kutafakari kipengele cha tatu jinsi ya kuwahudumia wajane, na neno linalotumika ni kuwaheshimu wajane walio wajane kweli kweli.

Uwaheshimu wajane walio wajane kweli kweli

1Timotheo 5:1-5 “Mzee usimkemee, bali umwonye kama baba; na vijana kama ndugu; wanawake wazee kama mama; wanawake vijana kama ndugu wa kike; katika usafi wote. Uwaheshimu wajane walio wajane kweli kweli. Lakini mjane akiwa ana watoto au wajukuu, na wajifunze kwanza kuyatenda yaliyo wajibu wao kwa jamaa zao wenyewe, na kuwalipa wazazi wao. Kwa kuwa hili lakubalika mbele za Mungu. Basi yeye aliye mjane kweli kweli, ameachwa peke yake, huyo amemwekea Mungu tumaini lake, naye hudumu katika maombi na sala mchana na usiku.”

Ni muhimu kujiuliza kwanini Paulo mtume anamuagiza Timotheo kuwaheshimu wajane walio wajane kweli kweli ni nini hasa maana yake? 

Kuwaheshimu – Neno kuwaheshimu kwa kiyunani hapa ni “timaō” ambalo maana yake ni “fix a valuation upon” yaani kuwapa uthamani, uwathamini, wawe wamekidhi vigezo, wawe wamefuzu, uwatambue “Give them a proper recognition” uwape heshima inayostahili, kwa hiyo Paulo mtume alikuwa anamuagiza Timotheo kama mwangalizi wa makanisa kule Efeso kuweka orodha yenye vigezo rasmi vya wajane wanaostahili kutambuliwa na kusaidiwa na kanisa wajane hao walijihusisha na huduma ya kanisa moja kwa moja baada ya kufiwa na waume zao, walijihusisha na maombi kanisani, wajane hao walikuwa ni wale ambao Paulo anawaita wajane kweli kweli yaani ni wajane wasio na mtu wa kuwasaidia, na wajane hao walipitia katika mchujo wenye vigezo kadhaa, na wamefuzu mtihani wa maisha ya uaminifu


Wajane kweli kweli - walikuwa ni wale wasiokuwa na watoto wala wajukuu wala ndugu wa kuwasaidia kabisa 

1Timotheo 5:3-4 “Uwaheshimu wajane walio wajane kweli kweli. Lakini mjane akiwa ana watoto au wajukuu, na wajifunze kwanza kuyatenda yaliyo wajibu wao kwa jamaa zao wenyewe, na kuwalipa wazazi wao. Kwa kuwa hili lakubalika mbele za Mungu. Basi yeye aliye mjane kweli kweli, ameachwa peke yake, huyo amemwekea Mungu tumaini lake, naye hudumu katika maombi na sala mchana na usiku.”


Walikuwa ni wajane ambao wanamtegemea Mungu na wanaishi maisha ya maombi kazi yao ni kuomba kwaajili ya kanisa, wanamuombea mchungaji, na huduma zote za kikanisa  na hudumu katika huduma hiyo.

 

1Timotheo 5:5 “Basi yeye aliye mjane kweli kweli, ameachwa peke yake, huyo amemwekea Mungu tumaini Lake, naye hudumu katika maombi na sala mchana na usiku.”


Luka 2:36-38 “Palikuwa na nabii mke, jina lake Ana, binti Fanueli, wa kabila ya Asheri, na umri wake ulikuwa miaka mingi, alikuwa amekaa na mume miaka saba baada ya uanawali wake. Naye ni mjane wa miaka themanini na minne; haondoki katika hekalu, ila huabudu usiku na mchana kwa kufunga na kuomba. Huyu alitokea saa ile ile akamshukuru Mungu, na wote waliokuwa wakiutarajia ukombozi katika Yerusalemu akawatolea habari zake.


Walikuwa ni wajane ambao waliishi maisha matakatifu na kujiepusha na lawama hawakuruhusu miili yao iwake tamaa na hawakuwa na mpango wa kuolewa tena bali waliishi maisha ya utauwa, tumaini lao ni Yesu. 


1Timotheo 5:5-7 “Basi yeye aliye mjane kweli kweli, ameachwa peke yake, huyo amemwekea Mungu tumaini lake, naye hudumu katika maombi na sala mchana na usiku. Bali, yeye asiyejizuia nafsi yake amekufa ingawa yu hai.Mambo hayo pia uyaagize, ili wasiwe na lawama.


Walikuwa ni wajane ambao sio wasichana sio wale wanaotamani kuolewa tena bali ni wajane ambao umri wao ni mkubwa na hawahitaji mume tena kwa hiyo Paulo alishauri ikiwezekana wawe na miaka sitini kwenda juu  na wale wanaojisikia kuolewa tena alisema waolewe wawe na nyumba zao.


1Timotheo 5:9-14 “Mjane asiandikwe isipokuwa umri wake amepata miaka sitini; naye amekuwa mke wa mume mmoja; naye ameshuhudiwa kwa matendo mema; ikiwa amelea watoto, ikiwa amekaribisha wageni, ikiwa amewaosha watakatifu miguu, ikiwa amewasaidia wateswao, ikiwa amefuata kwa bidii kila tendo jema. Bali wajane walio vijana ukatae kuwaandika hao, maana, wakizidiwa na tamaa kinyume cha Kristo, wataka kuolewa; nao wana hukumu kwa kuwa wameiacha imani yao ya kwanza. Tena, pamoja na hayo, hujifunza kuwa wavivu, wakizunguka-zunguka nyumba kwa nyumba; wala si wavivu tu, lakini ni wachongezi na wadadisi, wakinena maneno yasiyowapasa. Basi napenda wajane, ambao si wazee, waolewe, wazae watoto, wawe na madaraka ya nyumbani; ili wasimpe adui nafasi ya kulaumu.”


Kutumia vibaya mazingira magumu ya wajane – Kuwaheshimu wajane pia kulikuwa na maana ya kutoyatumia vibaya mazingira yao ya uhitaji kwa faida, Yesu Kristo aliwahi kuwalaumu Mafarisayo ambao kwa sababu za kidini waliyatumia mazingira yao ya kidini kuwatembelea wajane na kuonyesha kama wanawahurumia lakini wakiwa na nia ovu, au nia ya kutumia mazingira ya kidini kufunika uovu uliokuwa katika mioyo yao, na katika namna ya wazi walikuwa wakisali sala ndeefu sana ili kujiziba kwa jamii ya kuwa wanawajali wajane lakini kumbe walikuwa wanataka kuyatumia mazingira yao magumu kwa nia ovu, kwa hiyo katazo la Kristo ni kuwa mafarisayo walikuwa wanaonekana kama wanajali na kuheshimu sana wajane lakini ukweli ni kuwa walikuwa wanatumia mazingira magumu waliyo nayo wajane kwa faida zao, aidha kwaajili ya kupikiwa na kuhudumiwa ili wale, au kwaajili ya kupata tiba za kihisia kutoka kwa wajane hao, na mengine hatuyasemi kwa sababu Yesu mwenyewe hakuyasema, kwa hiyo utembeleo wao kwa nje ungeonekana kuwa ni wa kidini lakini kwa ndani walikuwa wanatengeneza mazigira ya kuleta faraja zisizokuwa za kiungu, kwa msingi huo watu wa Mungu hatupaswi kuwatumia wajane kwa misingi ya kufaidika kwetu kutoka kwao bali kwaajili ya utukufu wa Mungu, ukimtembelea Mjane huku ukiwa una nia nyingine mume wao ambaye ni Mungu anakuona!


Mathayo 23:14 “[Ole wenu waandishi na Mafarisayo, wanafiki! Kwa kuwa mnakula nyumba za wajane, na kwa unafiki mnasali sala ndefu; kwa hiyo mtapata hukumu iliyo kubwa zaidi.]

 

Hitimisho:


Neno la Mungu limeonyesha mkazo mkubwa sana na wa muhimu kuhusu kuwahudumia wajane na kuainisha kundi la wajane wanaopaswa kuhudumiwa lakini vile vile limetoa vigezo kwa wajane wanaojulikana katikia maandiko kama wajane walio wajane kweli kweli, Maandiko yanaelezea kuwa wao ni wa Muhimu na kwamba wanahitaji kupendwa, kujaliwa, kusaidiwa, kutiwa moyo na kulindwa, kwa kuwa kanisa tumepewa wajibu na agizo la Mungu ni pana uko umuhmu wa kutokulisahau jambo hili na hivyo Roho wa Mungu anataka tulikumbuke hili ili tuweze kujipatia Baraka zinazokusudiwa, kwa kuwajali na kushughulika nao tunajiweka katika nafasi ya Kristo inayoonyesha kuwa kanisa linajali, kwa hiyo pamoja na maagizo mengine hatupaswi kujisahau kama kanisa na kufumbia macho swala ambalo Mungu amelipa kipaumbele, Mungu mwenyewe amejionyesha kujishughulisha na wajane katika namna ya kipekee, Mungu aliwahudumia wajane kadhaa kwa miujiza mikubwa ili kutimiza mahitaji yao, wajane wakikuombea mtumishi wa Mungu, ujue ya kuwa Mungu anaheshimu sana maombi yao na kuwasikiliza sana, kila mtumishi wa Mungu anahitaji kuwa na waombezi wanaomuombea usiku na mchana unapofikiri kuhusu watu wa kukuombea maana yake unapaswa kuwafikiri wajane. Jicho na sikio la Mungu linawasikiliza sana kama tu endapo watasimama katika zamu yao. Kwa hiyo unaweza kuwa na timu ya maombi na kupa jina Ana binti Fanuel na ukawa na wajane wanaofanya kazi ya kuombea huduma mbalimbali lakini zaidi sana Mchungaji wa kanisa la mahali pamoja bila kusahau maombi ya wengine. 


Eliya alikaa pamoja na mjane wa sarepta, tukio ambalo hata Yesu alilithibitisha 1Wafalme 17:8-24 “Neno la Bwana likamjia, kusema, Ondoka, uende Sarepta, ulio mji wa Sidoni, ukae huko. Tazama, nimemwagiza mwanamke mjane wa huko akulishe. Basi, akaondoka, akaenda Sarepta; hata alipofika langoni pa mji, kumbe! Mwanamke mjane alikuwako akiokota kuni; akamwita, akamwambia, Niletee, nakuomba, maji kidogo chomboni nipate kunywa. Alipokuwa akienda kuleta, akamwita akasema, Niletee, nakuomba, kipande cha mkate mkononi mwako. Naye akasema, Kama Bwana, Mungu wako, aishivyo, sina mkate, ila konzi ya unga katika pipa, na mafuta kidogo katika chupa; nami ninaokota kuni mbili ili niingie nijipikie nafsi yangu na mwanangu, tuule tukafe. Eliya akamwambia, Usiogope; enenda ukafanye kama ulivyosema; lakini unifanyie kwanza mkate mdogo ukaniletee; kisha ujifanyie nafsi yako na mwanao. Kwa kuwa Bwana, Mungu wa Israeli, asema hivi, Lile pipa la unga halitapunguka, wala ile chupa ya mafuta haitaisha, hata siku ile Bwana atakapoleta mvua juu ya nchi. Basi akaenda, akafanya kama alivyosema Eliya; na yeye mwenyewe, na Eliya, na nyumba yake, wakala siku nyingi. Lile pipa la unga halikupunguka, wala ile chupa ya mafuta haikuisha, sawasawa na neno la Bwana alilolinena kwa kinywa cha Eliya. Ikawa, baada ya hayo, mwana wake yule mwanamke, bibi wa nyumba ile, akaugua; ugonjwa wake ukazidi hata akawa hana pumzi tena. Akamwambia Eliya, Nina nini nawe, Ee mtu wa Mungu? Je! Umenijia ili dhambi yangu ikumbukwe, ukamwue mwanangu? Akamwambia, Nipe mwanao. Akamtoa katika kifua chake, akamchukua juu chumbani mle alimokaa mwenyewe, akamlaza kitandani pake. Akamwomba Bwana, akanena, Ee Bwana, Mungu wangu, je! Umemtenda mabaya mjane huyu ninayekaa kwake hata kumfisha mwanawe. Akajinyosha juu ya mtoto mara tatu, akamwomba Bwana, akanena, Ee Bwana, Mungu wangu, nakusihi, roho ya mtoto huyu imrudie ndani yake tena. Bwana akaisikia sauti ya Eliya; na roho ya mtoto ikamrudia, akafufuka. Eliya akamtwaa mtoto, akamchukua toka orofani mpaka chini ya nyumba ile, akampa mama yake. Eliya akanena, Tazama, mwanao yu hai. Mwanamke akamwambia Eliya, Sasa najua ya kuwa wewe ndiwe mtu wa Mungu, na ya kuwa neno la Bwana kinywani mwako ni kweli.”


Elisha alimhudumia mjane aliyekuwa na deni 2Wafalme 4:1-7 “Basi, mwanamke mmoja miongoni mwa wake za wana wa manabii alimlilia Elisha, akasema, Mtumishi wako mume wangu amekufa; nawe unajua ya kuwa mtumishi wako alikuwa mcha Bwana; na aliyemwia amekuja ili ajitwalie wana wangu wawili kuwa watumwa. Elisha akamwambia, Nikufanyie nini? Niambie; una kitu gani nyumbani? Akasema, Mimi mjakazi wako sina kitu nyumbani, ila chupa ya mafuta. Akasema, Nenda, ukatake vyombo huko nje kwa jirani zako wote, vyombo vitupu; wala usitake vichache. Kisha uingie ndani, ukajifungie mlango wewe na wanao, ukavimiminie mafuta vyombo vile vyote; navyo vilivyojaa ukavitenge. Basi akamwacha, akajifungia mlango yeye na wanawe; hao wakamletea vile vyombo, na yeye akamimina. Ikawa, vilipokwisha kujaa vile vyombo, akamwambia mwanawe, Niletee tena chombo. Akamwambia, Hakuna tena chombo. Mafuta yakakoma. Ndipo akaja akamwambia yule mtu wa Mungu. Naye akasema, Enenda ukayauze mafuta haya, uilipe deni yako; nayo yaliyosalia uyatumie wewe na watoto wako.”


Na Yesu alimuhudumia mjane aliyekuwa na msiba Luka 7:11-16 “Baadaye kidogo alikwenda mpaka mji mmoja uitwao Naini, na wanafunzi wake walifuatana naye pamoja na mkutano mkubwa. Na alipolikaribia lango la mji, hapo palikuwa na maiti anachukuliwa nje, ni mwana pekee wa mamaye ambaye ni mjane, na watu wa mjini wengi walikuwa pamoja naye.Bwana alipomwona alimwonea huruma, akamwambia, Usilie. Akakaribia, akaligusa jeneza; wale waliokuwa wakilichukua wakasimama. Akasema, Kijana, nakuambia, Inuka. Yule maiti akainuka, akaketi, akaanza kusema. Akampa mama yake.Hofu ikawashika wote, wakamtukuza Mungu, wakisema, Nabii mkuu ametokea kwetu; na, Mungu amewaangalia watu wake.”  

Wewe na mimi tunafanya nini kuhusu wajane wanaotuizungika katika jamii ya kanisa la mahali pamoja Uongezewe neema 

Na Rev. Innocent Samuel Kamote

Mkuu wa wajenzi mwenye Hekima

Wewe nawe utakuwa kama mmoja wa wapumbavu?


2Samuel 13:11-13 “Naye alipokwisha kuileta karibu naye, ili ale, Amnoni akamkamata, akamwambia, Njoo ulale nami, ndugu yangu. Naye akamjibu, La, sivyo, ndugu yangu, usinitenze nguvu; kwani haifai kutendeka hivi katika Israeli; usitende upumbavu huu. Nami nichukue wapi aibu yangu? Wewe nawe utakuwa kama mmoja wa wapumbavu wa Israeli. Basi, sasa, nakusihi, useme na mfalme; kwa maana hatakukataza kunioa.”      

   



Utangulizi

Mojawapo ya tatizo ambalo limeleta majuto makubwa sana duniani na kuwaingiza wanadamu wengi kwenye changamoto mbalimbali ni pamoja na Upumbavu!, amini usiamini upumbavu umegharimu maisha ya watu wengi sana, na ni kupitia upumbavu aidha wa kwetu wenyewe au wa mtu mwingine, wengi wetu tumejikuta katika matatizo na changamoto zilizogharimu maswala kadhaa katika maisha, na ndio maana unaweza kuona maandiko matakatifu yakisisitiza sana umuhimu wa kuitafuta hekima kwa gharama yoyote ile kwa sababu hekima ni bora sana kuliko madini yoyote yale ya thamani zikiwemo rubi au marijani, Hekima inasimama kama njia ya kutusaidia kuvuka katika dunia hii salama.

Mithali 8:10-11 “Pokea mafundisho yangu, wala si fedha, Na maarifa kuliko dhahabu safi. Maana hekima ni bora kuliko marijani; Wala vyote vinavyotamanika havilingani nayo.”

Kwa msingi huo tunapojifunza somo hili lenye kichwa “Wewe nawe utakuwa kama mmoja wa wapumbavu?” Maana yake ni nini? Maana yake leo tutazungumzia kwa kina na mapana na marefu jinsi tunavyoweza kukwepa kufanya upumbavu tukiwa hapa duniani na hatimaye kuona umuhimu wa kumuomba Mungu na kuifuata njia ya Hekima ili tuweze kufanikiwa katika maisha haya  na yale yajayo, tutajifunza somo hili Wewe nawe utakuwa kama mmoja wa wapumbavu ? kwa kuzingatia vipengele vitatu viafuatavyo:-

·         Maana ya neno Upumbavu

·         Wewe nawe utakuwa kama mmoja wa wapumbavu?

·         Chagua Hekima!

Maana ya neno Upumbavu

Neno upumbavu katika lugha ya kiingereza linaelezewa kwa misamiati mingi sana kama vile fool, lacking of good sense, lacking of good judgement, unwise, stupid, silly, Idiotic, na kadhalika, lakini neno maarufu sana linalotumika katika Biblia hususani agano la kale ambalo limeletwa kwetu kwa lugha ya kiebrania ni neno nãbhãl  neno hilo kimsingi katika tamaduni za kiebrania linachukuliwa kama mtu aliyekosa hekima au mtu aliyepuuzia hekima, mtu asiye na uadilifu, mtu baradhuli, mtu muovu, mtu mbaya, mtu asiyetenda haki, mtu mwenye kuaibisha, mtu anayezungumza pumba, au mtu asiye muungwana, aliekosa uungwana au asiyefunzwa uungwana, mtu wa hila, asiye na akili, au mtu mwenye akili na hekima akifanya jambo la kushangaza kinyume na akili yake au hekima au njia ya Mungu, kwa hiyo katika mtazamo wa kiungu kufanya upumbavu ni kufanya jambo ambali liko kinyume na neno.  

Isaya 32:5-8 “Mpumbavu hataitwa tena mwungwana, wala ayari hatasemwa kwamba ni karimu. Maana mpumbavu atanena yaliyo upumbavu, na moyo wake utafanya maovu, ili kutenda hila na kusema yasiyo kweli juu ya Bwana, ili kuziacha nafsi za watu wenye njaa hazina kitu, na kukikomesha kinywaji chake mwenye kiu. Tena vyombo vyake ayari ni vibaya; hutunga hila mbaya, ili kuwaangamiza wanyonge kwa maneno ya uongo, mtu mhitaji ajaposema maneno yenye haki. Bali mwungwana huwaza mambo ya kiungwana, naye hushika sana mambo ya kiungwana.”

Kwa hiyo katika maandiko, mtu asipofikiri katika kutenda kwake, au akifanya maamuzi mabaya na hata kufikiri vibaya maana yake ametenda kwa upumbavu, na jambo hilo linaweza kutugharimu katika maisha yetu kimwili na kiroho.

2Samuel 24:9-10 “Naye Yoabu akamtolea mfalme jumla ya hesabu ya watu; nao walikuwa wa Israeli mashujaa wenye kufuta panga mia nane elfu; nao wa Yuda walikuwa watu mia tano elfu. Ndipo moyo wake Daudi ukamchoma baada ya kuwahesabu hao watu. Naye Daudi akamwambia Bwana, Nimekosa sana kwa haya niliyoyafanya; lakini sasa, Ee Bwana, nakusihi uuondolee mbali uovu wa mtumishi wako; kwani nimefanya upumbavu kabisa.”        

Kwa hiyo lugha upumbavu katika maandiko inaweza kuwa na upana wa kiharibiko zaidi ya kukosa maarifa, au ukosefu wa ustaarabu na kama mwanadamu hatakuwa makini mtu awaye yote yule, wa ngazi yoyote ile anaweza kujikuta anafanya upumbavu! Bwana ampe neema kila mmoja wetu ili tusiwe miongoni mwa watu watakaofanya upumbavu na kujutia katika maisha yetu, Katika jina la Yesu Kristo ameen!

Wewe nawe utakuwa kama mmoja wa wapumbavu?

Wakati wowote ule tunapofanya jambo ambalo limeagizwa katika neno la Mungu na lina uhusiano na uadilifu hapo tunatenda kwa hekima, na wakati wowote ule tunapofanya jambo ambalo liko kinyume na mapenzi ya Mungu na swala zima la uvunjifu wa uadilifu maana yake tunakuwa tumetenda kwa upumbavu, kwa hiyo upumbavu ni dhambi, upumbavu ni ujinga na upumbavu unaweza kutuweka pabaya, upumbavu unaweza kuyagharimu maisha yetu na ya wengine, na kwa kweli tukiruhusu, wivu, chuki, choyo, ubinafsi, kupenda fedha, kupenda madaraka, kujivuna kutembea kwa kiburi, na kadhalika na hayo yakatawala nafsi zetu ni rahisi sana kujikuta tumefanya upumbavu, kwa hiyo utaweza kuona kuwa dhambi na upumbavu ni mapacha wanaotembea kwa ukaribu sana  na tuwapo duniani  tunapaswa kujihadhari sana tusifanye upumbavu, ili tuweze kuishi kwa Amani.

Katika andiko letu la Msingi, ambalo Roho Mtakatifu Mwalimu mkuu alinipa na ndiko nilikopata kichwa cha ujumbe wa somo hili, tunasoma habari za Amnoni kijana aliyejawa na tamaa na kumpenda dada yake waliozaliwa mama tofauti lakini kwa baba mmoja, kijana huyu alimtamani sana dada yake na kiasi ambacho aliandaa njama za kutaka kumbaka, dada huyu alimshauri vizuri kwamba kama unanipenda unaweza kuzungumza na mfalme baba yao na hatakuzuia kunioa, lakini yeye akizidiwa na tamaa aliendelea na mpango wake wa kutaka kumbaka, dada yake aliyeonekana kuwa na busara sana alimshauri kuwa kwa kutumia njia anayotaka kuitumia atakuwa kama mojawapo ya wapumbavu katika Israel, yaani licha ya kuwa amefanya dhambi lakini atakuwa amefanya upumbavu, hii maana yake ni nini? wakati wote tunapoacha kutumia busara katika jambo lolote lile na tukaachia hisia zetu na tamaa ya mioyo yetu ituongoze maana yake au kinyume chake tunachagua njia ya kipumbavu na swali hili litatuhusu wewe nawe utakuwa kama mmoja wa wapumbavu?, maandiko matakatifu yamejaa mifano mingi ya watu waliotenda kwa upumbavu ambayo sisi hatupaswi kuiigia, kwani yaliandikwa kwa kusudi la kutupa hekima sisi tunaoishi miisho ya zamani hizi ili tusifanye upumbavu, kwa mfano:-

1.       Ukiwaza moyoni kuwa hakuna Mungu – Maandiko yanaonya kuwa sio kusema tu lakini mtu awaye yote ambaye anawaza moyoni mwake kuwa hakuna Mungu kibiblia huyo ni mpumbavu, hajishughulishi kumtafuta Mungu, haamini kama Mungu yupo, huyo ni mtenda maovu, awaye yote yule ambaye anaishi kana kwamba hakuna Mungu naye ni mpumbavu, wote wanaoishi kwa ukaidi wakikataa miongozo ya Mungu, wakilikataa neno la Mungu, wakiwa hawamtafuti Mungu na wanaishi sawa tu mawazo yao hao wanakuwa wamekengeuka na jumla yaw azo la kimungu kwao katika maandiko ni kuwa wamepumbazika.

Zaburi 14:1-3 “Mpumbavu amesema moyoni, Hakuna Mungu; Wameharibu matendo yao na kuyafanya chukizo, Hakuna atendaye mema. Toka mbinguni Bwana aliwachungulia wanadamu, Aone kama yuko mtu mwenye akili, Amtafutaye Mungu. Wote wamepotoka, wameoza wote pamoja, Hakuna atendaye mema, La! Hata mmoja.

Zaburi 53:1-3 “Mpumbavu amesema moyoni, Hakuna Mungu; Wametenda uovu wa ufisadi na kuchukiza, Hakuna atendaye mema. Toka mbinguni MUNGU aliwachungulia wanadamu, Aone kama yuko mtu mwenye akili, Amtafutaye Mungu.Kila mtu amepotoka, wameoza wote pamoja, Hakuna atendaye mema, La! Hata mmoja.

2.       Anayeshauri mtu amwache Mungu – Wako watu ambao katika namna ya kushangaza sana wanaweza kukushauri umwache Mungu, au utafute msaada kwa miungu mingine kwa sababu ya changamoto unazozipitia na misimamo yako katika kumuamini Mungu mtu anayefanya hivyo au kutoa ushauri wa namna hiyo katika maandiko anatajwa kama mtu anayezungumza upumbavu au pumba. Aidha mtu awaye yeto akikubali kuyategemea mawazo yake na njia zake au njia za kibinadamu huyu naye anatenda kwa upumbavu

Ayubu 2:7-10 “Basi Shetani akatoka mbele za uso wa Bwana, akampiga Ayubu na majipu mabaya tangu wayo wa mguu hata utosi wa kichwa. Naye akashika kigae cha kujikunia; akaketi majivuni. Ndipo mkewe akamwambia, Je! Wewe hata sasa washikamana na utimilifu wako? Umkufuru Mungu, ukafe. Lakini yeye akamwambia, Wewe wanena kama mmoja wa hao wanawake wapumbavu anenavyo. Je! Tupate mema mkononi mwa Mungu, nasi tusipate na mabaya? Katika mambo hayo yote Ayubu hakufanya dhambi kwa midomo yake.”  

3.       Kuondoka bila kuaga – Umekaa na mtu kwa muda mrefu katika maisha yako, au mahali ambapo ulikuwa unafanya kazi, alafu ukaamua kuondoka bila kuaga, au kutokumuaga baba yako wa kiroho, na kuamua kutoroka, bila kuagana kwa Amani na kubarikiana tendo hilo kadhalika linaweza kuwa sio dhambi lakini sio la kiungwana  wala kistaarabu kwa hivyo katika maandiko ukilifanya unahesabika kuwa umefanya upumbavu.

Mwanzo 31:26-28 “Labani akamwambia Yakobo, Umefanya nini? Umenihadaa, ukawachukua binti zangu kama mateka waliotwaliwa kwa upanga. Mbona umekimbia kwa siri ukanihadaa, wala hukuniambia, nipate kuagana nawe uende zako kwa furaha, na nyimbo, na ngoma, na kinubi? Wala hukuniacha niwabusu wanangu, na binti zangu; basi umetenda upumbavu.”

4.       Kulala na binti ya watu kabla ya kumchumbia au kumuoa – kimaandiko unapolala na binti ya watu na ukambikiri, kabla ya kumuoa kwa madai kuwa utamuoa baadaye jambo la namna hii ni la kipumbavu katika tamaduni za kimaandiko na Israel. Huwezi kuishi kama mwana ndoa kabla ya ndoa kwa kufanya hivyo unajidhihirisha namna ambavyo umekosa adabu, umekosa heshima, umekosa maarifa huna hekima na umefanya upumbavu.

Mwanzo 34:1-7 “Basi Dina, binti Lea, ambaye Lea alimzalia Yakobo, akatoka kuwaona binti za nchi. Shekemu, mwana wa Hamori, Mhivi, mkuu wa nchi, akamwona akamtwaa, akalala naye, akambikiri. Moyo wake ukaambatana na Dina binti Yakobo, akampenda huyu msichana, akasema na huyu msichana kwa maneno mazuri. Shekemu akamwambia Hamori, babaye, akasema, Unipatie msichana huyu awe mke wangu. Basi Yakobo akasikia ya kwamba amembikiri Dina, binti yake. Na wanawe walikuwako pamoja na wanyama wake nyikani. Yakobo akanyamaza, hata walipokuja. Akatoka Hamori, babaye Shekemu, kumwendea Yakobo, aseme naye. Wanawe Yakobo waliposikia hayo, wakaja kutoka nyikani; nao wakasikitika sana, wakakasirika mno, kwa sababu amefanya upumbavu katika Israeli kwa kulala na binti Yakobo, neno lisilojuzu kutendeka.”           

5.       Kumdhalilisha mwanamke – tendo la mtu kumuoa mwanamke aliye bikira, kisha akafika ndani na ukamchukia kisha kumsingizia kuwa eti hakuwa na ubikira tendo la kumdhalilisha na kumuaibisha mwanamke katika Israel na katika swala zima la uadilifu ni kutenda upumbavu.

Kumbukumbu 22:13-21 “Mtu akitwaa mke, akamwingilia na kumchukia, kisha akamshitaki mambo ya aibu kumzushia jina baya, akasema, Nimemtwaa mwanamke huyu, nami nilipomkaribia sikuona kwake alama za ubikira; ndipo babaye yule kijana na mamaye watakapotwaa alama za yule kijana za ubikira, wawatolee wazee wa mji langoni; na baba yake yule kijana awaambie wazee, Mwanamume huyu nilimpa binti yangu awe mkewe, naye amchukia; angalieni, amemwekea mambo ya aibu, asema, Sikuona kwa binti yako alama za ubikira, nazo hizi ndizo alama za binti yangu za ubikira. Na wayakunjue yale mavazi mbele ya wazee wa mji. Basi wazee wa mji ule na wamtwae yule mtu mume na kumrudi, wamtoze shekeli mia za fedha, wampe babaye yule kijana, kwa kuwa amemzulia jina baya mwanamwali wa Israeli; naye awe mkewe; hana ruhusa ya kumwacha siku zake zote. Lakini likiwa ni kweli neno hili, la kutoonekana kwake yule kijana alama za ubikira; na wamtoe nje yule kijana mlangoni pa nyumba ya baba yake, na waume wa mji wake wampige kwa mawe hata afe; kwa vile alivyofanya upumbavu katika Israeli, kwa kufanya ukahaba katika nyumba ya baba yake; ndivyo utakavyoondoa uovu katikati yako.”

               

6.       Awaye yote anayeiba – Maandiko matakatifu yanaagiza kuwa tusiibe, lakini sio hivyo tu kila mmoja anaagizwa kuyatii maagizo ya Bwana na kulishika agano lake, kufanya jambo kinyume na hayo ni kufanya upumbavu, mtu anayeiba ni mpumbavu, amechagua njia isiyo ya kiungwana.

Yoshua 7:11-15 “Israeli wamefanya dhambi, naam, wamelivunja agano langu nililowaagiza; naam, wametwaa baadhi ya vitu vilivyowekwa wakfu; tena wameiba, tena wameficha na kuvitia pamoja na vitu vyao wenyewe. Ndiposa wana wa Israeli hawawezi kusimama mbele ya adui zao; wakawapa visogo adui zao, kwa sababu wamelaaniwa; mimi sitakuwa pamoja nanyi tena, msipokiharibu kitu kile mlicho nacho kilichowekwa wakfu. Haya! Inuka, uwatakase watu, ukaseme, Jitakaseni, mwe tayari kesho; maana Bwana, Mungu wa Israeli, asema hivi; Kitu kilichowekwa wakfu kiko katikati yako, Ee Israeli; huwezi kusimama mbele ya adui zako, hata mtakapokiondoa kile mlicho nacho kilichowekwa wakfu. Basi asubuhi mtaletwa karibu nami kabila kwa kabila; kisha itakuwa ya kwamba kabila ile atakayoitwaa Bwana itakaribia jamaa kwa jamaa; na jamaa ile atakayoitwaa Bwana itakaribia nyumba kwa nyumba; na nyumba ile atakayoitwaa Bwana itakaribia mtu kwa mtu. Tena itakuwa ya kwamba yeye atakayetwaliwa, naye anacho kitu kile kilichowekwa wakfu, atateketezwa kwa moto, yeye na vitu vyote alivyo navyo; kwa sababu amelivunja agano la Bwana, na kwa sababu ametenda upumbavu katika Israeli.”

7.       Kumbaka mwanamke -  Kumbaka mwanamke na kumuingilia kinyume cha maumbile, sio tu kuwa ni dhambi, lakini vilevie ni upumbavu, katika jamii, jambo hilo ni uovu ambao sio tu utakugharimu kufunguliwa mashitaka na kufungwa lakini kwa Mungu ni dhambi na ni uovu katika jamii.

Waamuzi 20:4-6 “Huyo Mlawi, huyo mume wa mwanamke aliyeuawa, akajibu na kusema, Mimi nilifikilia Gibea ulio wa Benyamini mimi na suria yangu, ili tulale. Nao watu waume wa Gibea wakaniondokea, na kuizingira hiyo nyumba pande zote juu yangu wakati wa usiku; walidhani kuniua, na suria wangu wakamtenza nguvu, hata amekufa.Basi nikamtwaa huyo suria yangu, na kumkata vipande, na kumpeleka katika nchi yote ya urithi wa Israeli; kwa sababu wametenda maovu makuu na upumbavu katika Israeli.”

8.       Tamaa na kutaka kulawiti ni upumbavu – jamii inapokuwa na watu ambao wanaona kuwa mapenzi ya jinsia moja kama jambo la kawaida maana yake jamii hiyo imepumbazika, usagaji ni upumbavu, ulawiti ni upumbavu, usagaji ni upumbavu, ni kukosa akili ni kukosa hekima kwa hiyo ukiiangalia dunia ya leo na swala zima la maovu yanayohusiana na ulawiti na tamaa ya aina hiyo utaweza kuwa na picha halisi kuwa watu hata pamoja na kuwa na elimu kubwa hivyo na marifa kuongezeka, dunia imekuwa na wapumbavu wengi sana.

Waamuzi 19:23-25 “Naye mtu mwenye nyumba akawatokea hapo nje, na kuwaambia, La, sivyo, ndugu zangu nawasihi msifanye uovu jinsi hii; kwa kuwa mtu huyu ameingia ndani ya nyumba yangu, msifanye upumbavu huu. Tazama, binti yangu yupo hapa, ni mwanamwali, na suria wake huyo mtu; nitawaleta hapa nje sasa nanyi watwezeni, na kuwatenda hayo myaonayo kuwa ni mema; lakini mtu huyu msimtende jambo la upumbavu namna hii. Lakini hao watu hawakukubali kumsikia; basi mtu huyo akamshika suria wake, na kumleta nje kwao; nao wakamjua, na kumtenda uovu usiku kucha hata asubuhi kisha kulipoanza kupambauka wakamwacha aende zake.”

Warumi 1:21-28 “kwa sababu, walipomjua Mungu hawakumtukuza kama ndiye Mungu wala kumshukuru; bali walipotea katika uzushi wao, na mioyo yao yenye ujinga ikatiwa giza. Wakijinena kuwa wenye hekima walipumbazika; wakaubadili utukufu wa Mungu asiye na uharibifu kwa mfano wa sura ya binadamu aliye na uharibifu, na ya ndege, na ya wanyama, na ya vitambaavyo. Kwa ajili ya hayo Mungu aliwaacha katika tamaa za mioyo yao, waufuate uchafu, hata wakavunjiana heshima miili yao. Kwa maana waliibadili kweli ya Mungu kuwa uongo, wakakisujudia kiumbe na kukiabudu badala ya Muumba anayehimidiwa milele. Amina. Hivyo Mungu aliwaacha wafuate tamaa zao za aibu, hata wanawake wakabadili matumizi ya asili kwa matumizi yasiyo ya asili; wanaume nao vivyo hivyo waliyaacha matumizi ya mke, ya asili, wakawakiana tamaa, wanaume wakiyatenda yasiyopasa, wakapata nafsini mwao malipo ya upotevu wao yaliyo haki yao.Na kama walivyokataa kuwa na Mungu katika fahamu zao, Mungu aliwaacha wafuate akili zao zisizofaa, wayafanye yasiyowapasa.”                   

9.       Kuropoka – nadhani umewahi kuishi na watu wanaoropoka, na utakuwa unajua madhara ya kuropoka, kuropoka ni kuzungumza kitu bila kufikiri, wako watu yaani kitakachomjia kichwani tu anakitekeleza kwa kusema au kuandika sms isiyofaa, unaweza kutuma ujumbe usiofaa kwa mke wa mtu, mume wa mtu, unaweza kuropoka mambo ya watu au siri za watu, au kutokwa na maneno yasiyo na maana kama mtu hana nidhamu katika kuzungumza kwake maana yake anashindwa kuudhibiti ulimi wake naye anaitwa mpumbavu

Mithali 14:3 “Katika kinywa cha mpumbavu mna fimbo ya kiburi, Bali midomo ya wenye hekima huwahifadhi. 

Mithali 12:15-16 “Njia ya mpumbavu imenyoka machoni pake mwenyewe; Bali yeye aliye na hekima husikiliza shauri. Ghadhabu ya mpumbavu hujulika mara; Bali mtu mwerevu husitiri aibu.”

10.   Kufanya dhambi – Kufanya dhambi ya aina yoyote ile kibiblia ilihesabika kuwa ni kufanya upumbavu, kwani kila dhambi licha ya kuwa uko msamaha wa Mungu na rehema zake lakini kwa kuwa Mungu ni mwenye haki wakati mwingine matokeo ya dhambi yanaweza kuendeleza madhara makubwa nje ya msamaha wa Mungu, mfano ukifanya uasherati ukapata mimba, na ukatubu kwa uasherati ule utasamehewa lakini mimba haitayeyuka kwa hiyo ulipaswa kufikiri kabla ya kutenda na kwa kutokufikiri umefanya upumbavu. Na au ukapata ukimwi, rehema za Mungu zinaweza kuwepo lakini na virusi vinaendelea kuwepo kwa sababu ulifanya upumbavu, hukutoa nafasi ya kufikiri kwa kina madhara unayoweza kuyapata. Kwa hiyo ni muhimu kukumbuka ya kuwa dhambi ina madhara yake na madhara yake ni mabaya sana katika maisha ya watu wote

Zaburi 38:3-5 “Hamna uzima katika mwili wangu Kwa sababu ya ghadhabu yako. Wala hamna amani mifupani mwangu Kwa sababu ya hatia zangu. Maana dhambi zangu zimenifunikiza kichwa, Kama mzigo mzito zimenilemea mno. Jeraha zangu zinanuka, zimeoza, Kwa sababu ya upumbavu wangu.”

Zaburi 69:3-5 “Nimechoka kwa kulia kwangu, Koo yangu imekauka. Macho yangu yamedhoofu Kwa kumngoja Mungu wangu. Wanaonichukia bure ni wengi Kuliko nywele za kichwa changu. Watakao kunikatilia mbali wamekuwa hodari, Adui zangu kwa sababu isiyo kweli. Hata mimi nalilipishwa kwa nguvu Vitu nisivyovichukua. Ee Mungu, unajua upumbavu wangu, Wala hukufichwa dhambi yangu.”

11.   Ukiruhusu hasira kukutawala – wako watu ambao kupitia hasira wamefanya mambo ya kijinga na kipumbavu na baadaye kujilaumu au kupata majuto, maandiko yanatutaka kujidhibiti, kujitia nidhamu, badala ya kujisifia kuwa wewe una hasira, hakikisha unajinidhamu kushindwa kufanya hivyo ni kuruhusu upumbavu.

Muhubiri 7:4-9 “Moyo wake mwenye hekima umo nyumbani mwa matanga, bali moyo wake mpumbavu umo nyumbani mwa furaha. Heri kusikia laumu ya wenye hekima, Kuliko mtu kusikia wimbo wa wapumbavu; Maana kama mlio wa miiba chini ya sufuria, Ndivyo kilivyo kicheko cha mpumbavu. Hayo nayo ni ubatili. Kweli jeuri humpumbaza mwenye hekima, Na rushwa huuharibu ufahamu. Heri mwisho wa neno kuliko mwanzo wake, Na mvumilivu rohoni kuliko mwenye roho ya kiburi. Usifanye haraka kukasirika rohoni mwako, Maana hasira hukaa kifuani mwa wapumbavu.”

12.   Kumtendea maovu mtu ambaye hana nia mbaya na wewe – wako watu wengine kwa sababu ya wivu tu wenye uchungu wanaweza kukutendea mabaya, au wanaweza kukusudia kutenda mabaya kwa watu ambao hawana nia wala wazo la kuwadhuru, kufanya jambo la namna hiyo ni machukizo sio kwa Mungu tu lakini ni upumbavu, kutafuta na kutaka kumdhuru mtu ambaye hana mpango wala nia ya kukudhuru.

1Samuel 26:18-21. “Akasema, Bwana wangu ananiwinda mimi mtumishi wake kwa sababu gani? Nimefanya nini mimi? Ni uovu gani nilio nao mkononi mwangu? Basi sasa, nakusihi, bwana wangu, mfalme, na asikie maneno ya mtumishi wake. Ikiwa ni Bwana aliyekuondokesha juu yangu, na akubali sadaka; bali ikiwa ni wanadamu, na walaaniwe mbele za Bwana; kwa sababu wamenifukuza leo, nisishikamane na urithi wa Bwana, wakisema, Enenda, katumikie miungu mingine.Basi sasa, isianguke damu yangu chini mbali na uso wa Bwana; maana mfalme wa Israeli ametoka ili kutafuta uhai wangu, kama vile mtu awindavyo kware mlimani.Ndipo Sauli akasema, Nimekosa; rudi, Daudi, mwanangu; maana sitakudhuru tena, kwa kuwa maisha yangu yalikuwa na thamani machoni pako leo; angalia, nimetenda upumbavu, nimekosa sana.”     

13.   Mtu anayefikiria maovu na mwenye mizaha - Maandiko yanataja vitu kadhaa vinavyomchukiza Mungu, ikiwa ni pamoja na moyo uwazao mabaya, yaani maswala hayo ni machukizo kwa Mungu, maana yake kule kufikiri na kuwaza namna ya kufanya maovu, ni kufikiri na kufanya dhambi hayo yanawekwa katika kundi moja la machukizo kwa Mungu, ambayo kimsingi nayo yanaitwa upumbavu katika maandiko kwa sababu moyoni ndiko chanzo cha kila kitu kibaya kwa hiyo kufikiri au kuwaza maovu ni kuwaza upumbavu na zaidi sana ikiwa ni pamoja na mizaha, kwa hiyo kila mmoja wetu ajichunge fikira zake na kujihadhari za mizaha.  

Mithali 6:16-19 “Kuna vitu sita anavyovichukia Bwana; Naam, viko saba vilivyo chukizo kwake. Macho ya kiburi, ulimi wa uongo, Na mikono imwagayo damu isiyo na hatia; Moyo uwazao mawazo mabaya; Miguu iliyo myepesi kukimbilia maovu;Shahidi wa uongo asemaye uongo; Naye apandaye mbegu za fitina kati ya ndugu.”

Mithali 24:9 “Fikira za mpumbavu ni dhambi, Na mwenye mzaha huwachukiza watu.”

14.   Mtu anayelipa maovu badala ya mema – kwa maana nyingine ni watu wasio na shukurani, wako watu ambao unaweza kuwatendea mema na kisha ukahitaji fadhili ndogo tu kutoka kwao lakini wakakulipa mabaya badala ya mema mfano wa aina hii ya upumbavu ndio uliofanywa na mtu mwenye kuitwa nabali ambayo ndio tafasiri ya somo hili Nabali maana yake mpumbavu ambaye alioa mwanamke muungwana au mwenye akili.

1Samuel 25:2-26 “Na huko Maoni kulikuwa na mtu mmoja, ambaye alikuwa na mali yake katika Karmeli; naye yule mtu alikuwa mkuu sana, mwenye kondoo elfu tatu na mbuzi elfu; naye alikuwa akiwakata manyoya kondoo zake huko Karmeli. Na jina la mtu huyo aliitwa Nabali; na jina la mkewe aliitwa Abigaili, na huyo mwanamke alikuwa mwenye akili njema, mzuri wa uso; bali yule mwanamume alikuwa hana adabu, tena mwovu katika matendo yake; naye alikuwa wa mbari ya Kalebu. Basi Daudi akasikia huko nyikani ya kuwa Nabali alikuwa katika kuwakata manyoya kondoo zake. Daudi akatuma vijana kumi, Daudi naye akawaambia hao vijana, Kweeni mwende Karmeli, na kumwendea huyu Nabali ili mnisalimie; na hivi ndivyo mtakavyomwambia huyu aishiye salama, Amani na iwe kwako, na amani nyumbani mwako, na amani kwao wote ulio nao. Nami sasa nimesikia ya kuwa una watu wanaokata manyoya kondoo zako; haya! Wachungaji wako wamekuwa pamoja nasi, wala hatukuwadhuru, wala hawakukosa kitu wakati wote walipokuwako huko Karmeli. Waulize vijana wako, nao watakuambia; basi na wakubaliwe vijana hawa machoni pako; maana tumekujia katika siku ya heri; uwape, nakusihi, cho chote kitakachokujia mkononi, uwape watumwa wako na mwanao Daudi. Basi walipofika vijana wake Daudi, wakamwambia Nabali sawasawa na maneno hayo yote kwa jina la Daudi, kisha wakanyamaza. Naye Nabali akawajibu wale watumishi wa Daudi, akasema, Huyu Daudi ni nani? Na mwana wa Yese ni nani? Siku hizi kuna watumwa wengi wanaomtoroka kila mtu bwana wake! Basi mimi je! Nitwae mkate wangu, na maji yangu, na machinjo yangu niliyowachinjia hao watu wangu wakatao manyoya kondoo zangu, na kuwapa watu ambao siwajui wametoka wapi? Basi vijana wake Daudi wakageuka, wakaenda zao, wakarudi, nao wakaja wakamwambia sawasawa na maneno hayo yote. Kisha Daudi akawaambia watu wake, Haya! Jifungeni kila mtu upanga wake. Nao wakajifunga kila mtu upanga wake; Daudi naye akajifunga upanga wake; nao wakapanda nyuma yake Daudi, wapata kama watu mia nne; na watu mia mbili wakakaa na vyombo vyao.Lakini kijana mmojawapo alimpasha habari Abigaili, mkewe Nabali, kasema, Tazama, Daudi alituma wajumbe kutoka nyikani waje ili kumsalimu bwana wetu, naye akawatukana. Walakini watu hawa walitutendea mema sana, wala hatukupata dhara, wala sisi hatukupotewa na kitu cho chote, wakati wote tulipofuatana nao, tulipokuwako mavueni; watu hao walikuwa boma kwetu usiku na mchana, wakati wote tulipokuwa nao tukiwachunga kondoo. Basi sasa ujue na kufikiri utakayotenda; kwa sababu yamekusudiwa mabaya juu ya bwana wetu, na juu ya nyumba yake yote; kwa kuwa yeye ni mtu asiyefaa kabisa, hata mtu hawezi kusema naye. Ndipo Abigaili akafanya haraka, akatwaa mikate mia mbili, na viriba viwili vya divai, na kondoo watano waliofanyizwa tayari, na vipimo vitano vya bisi, na vishada mia vya zabibu, na mikate ya tini mia mbili; akavipakia vitu hivi juu ya punda. Akawaambia vijana wake, Haya! Tangulieni mbele yangu; angalieni, mimi nawafuata. Ila hakumwambia mumewe, Nabali. Ikawa, alipokuwa amepanda punda wake, na kutelemka penye sitara ya mlima, tazama, Daudi na watu wake walikuwa wakishuka kumkabili; naye akawakuta. Basi Daudi alikuwa amesema, Hakika ni bure nilivyokuwa nikilinda nyikani yote aliyo nayo mtu huyu, asipotewe na kitu cho chote cha mali yake yote; naye amenilipa mabaya badala ya mema. Mungu naye awafanyie hivyo adui za Daudi, na kuzidi, nikimwachia katika wote walio wake hata mtoto mume mmoja, kutakapopambazuka asubuhi. Ndipo hapo Abigaili alipomwona Daudi, alifanya haraka kushuka juu ya punda wake, akamwangukia Daudi kifulifuli, akainama mpaka nchi. Akamwangukia miguuni pake, akasema, Juu yangu, bwana wangu, juu yangu mimi na uwe uovu; tafadhali mjakazi wako na anene masikioni mwako, nawe uyasikilize maneno ya mjakazi wako. Nakusihi, bwana wangu, wewe usimwangalie huyu mtu asiyefaa, yaani, Nabali; kwa maana kama lilivyo jina lake ndivyo alivyo yeye; jina lake ndilo Nabali, na upumbavu anao; lakini mimi, mjakazi wako, sikuwaona hao vijana wa bwana wangu aliowatuma. Basi sasa, bwana wangu, aishivyo Bwana, na iishivyo nafsi yako, kwa kuwa Bwana amekuzuia usimwage damu, tena usijilipize kisasi mkono wako mwenyewe, basi sasa adui zako, na hao wamtakiao bwana wangu mabaya, wawe kama Nabali.

15.   Mwanamke asiye na hekima – Biblia aidha pia ina maonyo mengi kuhusu mwanamke mcha Mungu, na mwenye hekima kuwa ni mwanamke anayeweza kusimamia nyumba yake vizuri, na maandiko yanaonyesha kuwa kama mwanamke hamchi Mungu nyumba yake haiwezi kusimama mwanamke asiye mcha Mungu anaweza kuhesabika kama mkaidi, asiyetaka kumtii Mumewe, hafundishiki, mbishi, mbinafsi, anayetawala nyumba, mchoyo kwa tendo la ndoa na anayeamua kumkomoa mumewe kwa tendo hilo, mvivu wa ibada, hajishushi, mumewe akipanda naye anapanda juu zaidi, anayependa usingizi, Mmbeya, hafanyi kazi kwa mikono yake mwenyewe, na majukumu ya mke anayapuuzia na kupenda starehe nyingine utaongezea mwenyewe mwanamke wa aina hiyo ndiye anayefikiriwa kuwa hana hekima na hivyo maandiko yanamuita mpumbavu.

Mithali 14:1-2 “Kila mwanamke aliye na hekima hujenga nyumba yake; Bali aliye mpumbavu huibomoa kwa mikono yake mwenyewe. Yeye aendaye kwa unyofu wake humcha Bwana; Bali aliye mkaidi katika njia zake humdharau.

Mithali 9:13-17 “Mwanamke mpumbavu hupiga kelele, Ni mjinga, hajui kitu.Hukaa mlangoni pa nyumba yake, Juu ya kiti mahali pa mjini palipoinuka, Apate kuwaita wapitao njiani, Waendao moja kwa moja katika njia zao. Kila aliye mjinga na aingie humu. Tena amwambia mtu aliyepungukiwa na akili, Maji yaliyoibiwa ni matamu, Na mkate ulioliwa kwa siri hupendeza.”

Mithali 21:9 “Ni afadhali kukaa katika pembe ya darini, Kuliko katika nyumba pana pamoja na mwanamke mgomvi.”

               

Mithali 21:19 “Ni afadhali kukaa katika nchi ya nyika; Kuliko na mwanamke mgomvi, mchokozi.”

               

Mithali 25:24 “Ni afadhali kukaa katika pembe ya darini, Kuliko katika nyumba pana pamoja na mwanamke mgomvi.

16.   Kutokumjua Mungu wala njia zake  Watu wanaweza kuwa na maarifa ya aina nyingine mfano maarifa ya kupanga ubaya, kufanya maovu, kutekeleza majungu, kuharibu mahusiano, lakini hawana maarifa wala akili ya kumtafuta Mungu, ziko nguvu za uovu ambazo watu wanazifanya ambazo kama zingeelekezwa katika kumtafuta Mungu na kuongeza maarifa ya kumjua Mungu watu wangekuwa mbali sana

Yeremia 4:22 “Kwa maana watu wangu ni wapumbavu, hawanijui; ni watoto waliopungukiwa na akili, wala hawana ufahamu; ni wenye akili katika kutenda mabaya, bali katika kutenda mema hawana maarifa.”

17.   Wanaoamini Manabii wa uongo – Wako manabii ambao kazi yao kubwa ni kuzungumza maneno ya kufariji watu, ilihali wakati mwingine suluhu ya uponyaji wa watu hao ni kuwaambia tu watubu dhambi zao, ziko changamoto nyingi sana duniani zinazosababishwa na dhambi kuliko hata wachawi na laana za ukoo, wakati mwingine mtu akisamehewa dhambi zake na uponyaji wake unakuja kama neno lake lisemavyo, akusamehe maovu yako yote, akuponya magonjwa yako yote, waambie watu kosa lao badala ya kuona maono ya ubatili na upumbavu, manabii wa uongo huona maono ya kipumbavu na hivyo kuzuia kuponywa kwako.

Maombolezo 2:13-14 “Nikushuhudie nini? Nikufananishe na nini, Ee Binti Yerusalemu? Nikusawazishe na nini, nipate kukufariji, Ee bikira binti Sayuni? Kwa maana uvunjifu wako ni mkuu kama bahari, Ni nani awezaye kukuponya? Manabii wako wameona maono kwa ajili yako Ya ubatili na upumbavu Wala hawakufunua uovu wako, Wapate kurudisha kufungwa kwako; Bali wameona mabashiri ya ubatili kwa ajili yako Na sababu za kuhamishwa.                

18.   Kutokulifanyia kazi neno la Mungu – kama watu wengi tungekuwa tunalitii neno la Mungu tungekuwa na mafanikio makubwa sana na ustawi mkubwa sana katika maswala yote ya mwili na roho lakini kwa bahati mbaya sana kulitii neno la Mungu limekuwa jambo gumu kwa kizazi hiki hata kama watu wanatii wengi huchagua maswala kadhaa ya kuyatii lakini neno la Mungu linatukumbusha kuyatii maagizo yote na kuyafanyia kazi maneno ya Mungu.

Yakobo 1:22-24 “Lakini iweni watendaji wa neno, wala si wasikiaji tu, hali mkijidanganya nafsi zenu.Kwa sababu mtu akiwa ni msikiaji wa neno tu, wala si mtendaji, mtu huyo ni kama mtu anayejiangalia uso wake katika kioo. Maana hujiangalia, kisha huenda zake, mara akasahau jinsi alivyo.

Mathayo 7:24-27 “Basi kila asikiaye hayo maneno yangu, na kuyafanya, atafananishwa na mtu mwenye akili, aliyejenga nyumba yake juu ya mwamba; mvua ikanyesha, mafuriko yakaja, pepo zikavuma, zikaipiga nyumba ile, isianguke; kwa maana misingi yake imewekwa juu ya mwamba. Na kila asikiaye hayo maneno yangu asiyafanye, atafananishwa na mtu mpumbavu, aliyejenga nyumba yake juu ya mchanga; mvua ikanyesha, mafuriko yakaja, pepo zikavuma, zikaipiga nyumba ile, ikaanguka; nalo anguko lake likawa kubwa.”

19.   Kujilinganisha na wengine – Katika maisha haya Mungu amemuumba kila mwanadamu akiwa na baraka tofauti na karama na vipawa tofauti, kwa hiyo kimaandiko mwanadamua anyejilinganisha na mwingine au kuipima nafsi yake akiilinganisha nay a mtu mwingine mtu huyo hana akili na ni mpumbavu, kwa mujibu wa maandiko, hatupaswi kamwe kujilinganisha na wengine kwa sababu kila mwanadamu Mungu amemuumba kwa namna na jinsi ya aina yake kwa uhodari mkubwa!

2Wakorintho 10:11-18 “Mtu kama huyo na afikiri hivi, ya kwamba jinsi tulivyo kwa maneno katika nyaraka tusipokuwapo, ndivyo tulivyo kwa matendo tukiwapo. Kwa kuwa hatuthubutu kujihesabu pamoja na baadhi yao wanaojisifu wenyewe, wala kujilinganisha nao; bali wao wenyewe wakijipima nafsi zao na nafsi zao, na wakijilinganisha nafsi zao na nafsi zao, hawana akili. Lakini sisi hatutajisifu zaidi ya kadiri yetu; bali kwa kadiri ya kipimo tulichopimiwa na Mungu, yaani, kadiri ya kufika hata kwenu. Maana hatujitanui nafsi zetu kupita kadiri yetu, kana kwamba hatuwafikii ninyi; kwa sababu tulitangulia kufika mpaka kwenu katika injili ya Kristo; wala hatujisifu zaidi ya kadiri yetu, yaani, katika taabu za watu wengine; bali tukiwa na tumaini ya kwamba, imani yenu ikuapo, tutakuzwa kwenu kwa kadiri ya kipimo chetu, na kupata ziada; hata kuihubiri Injili katika nchi zilizo mbele kupita nchi zenu; tusijisifu katika kipimo cha mtu mwingine kwa mambo yaliyokwisha kutengenezwa. Lakini, Yeye ajisifuye, na ajisifu katika Bwana. Maana mtu mwenye kukubaliwa si yeye ajisifuye, bali yeye asifiwaye na Bwana.”

20.   Kutokujitayarisha kwa Mungu -  watu wote duniani wanapaswa kujiandaa kwaajili ya kukutana na Mungu, na kujiandaa kwaajili ya ujio wa Bwana wetu Yesu Kristo mara ya pili duniani, na kunyakuliwa kwa kanisa, kuishi maisha ya vuguvugu na kujidanganya kunaweza kuja kutuletea majuto na kilio na kusaga meno, Yesu mara kadhaa alisisitiza jamii kujiandaa kwaajili ya Mungu na awaye yote ambaye atakosa mbingu atakuwa amekosa kwaajili ya upumbavu, Bwana amtunze kila mmoja wetu asiikose mbingu katika jina la Yesu Kristo.

Luka 12:16-21 “Akawaambia mithali, akisema, Shamba la mtu mmoja tajiri lilikuwa limezaa sana; akaanza kuwaza moyoni mwake, akisema, Nifanyeje? Maana sina pa kuyaweka akiba mavuno yangu.  Akasema, Nitafanya hivi; nitazivunja ghala zangu, nijenge nyingine kubwa zaidi, na humo nitaweka nafaka yangu yote na vitu vyangu. Kisha, nitajiambia, Ee nafsi yangu, una vitu vyema vingi ulivyojiwekea akiba kwa miaka mingi; pumzika basi, ule, unywe, ufurahi. Lakini Mungu akamwambia, Mpumbavu wewe, usiku huu wa leo wanataka roho yako! Na vitu ulivyojiwekea tayari vitakuwa vya nani? Ndivyo alivyo mtu ajiwekeaye nafsi yake akiba, asijitajirishe kwa Mungu.

Mathayo 25:1-13 “Ndipo ufalme wa mbinguni utakapofanana na wanawali kumi, waliotwaa taa zao, wakatoka kwenda kumlaki bwana arusi. Watano wao walikuwa wapumbavu, na watano wenye busara. Wale waliokuwa wapumbavu walizitwaa taa zao, wasitwae na mafuta pamoja nao; bali wale wenye busara walitwaa mafuta katika vyombo vyao pamoja na taa zao. Hata bwana arusi alipokawia, wote wakasinzia wakalala usingizi. Lakini usiku wa manane, pakawa na kelele, Haya, bwana arusi; tokeni mwende kumlaki. Mara wakaondoka wanawali wale wote, wakazitengeneza taa zao. Wale wapumbavu wakawaambia wenye busara, Tupeni mafuta yenu kidogo; maana taa zetu zinazimika. Lakini wale wenye busara wakawajibu, wakisema, Sivyo; hayatatutosha sisi na ninyi; afadhali shikeni njia mwende kwa wauzao, mkajinunulie.Na hao walipokuwa wakienda kununua, bwana arusi akaja, nao waliokuwa tayari wakaingia pamoja naye arusini; mlango ukafungwa.Halafu wakaja na wale wanawali wengine, wakasema, Bwana, Bwana, utufungulie. Akajibu akasema, Amin, nawaambia, siwajui ninyi. Basi kesheni, kwa sababu hamwijui siku wala saa.

Chagua Hekima!

Tungeweza kuchambua maswala mengi sana yanayozungumzia upumbavu lakini muda usingelitosha, ni ukweli ulio wazi ya kuwa maandiko yanatuonyesha wazi kuwa upumbavu ni tatizo na janga zito sana kuliko hata dhambi zenyewe, kwani hakuna dhambi ambayo utaifanya na isiwe kuwa hukufanya upumbavu, ziko tabia mbaya nyingi sana ambazo mtu akizitenda kimaandiko anaitwa amefanya upumbavu, swali kubwa la kujiuliza Je wewe nawe utakuwa kama mmoja wa wapumbavu? Kama hutaki neno la Mungu linatushauri kuchagua hekima na hii ndio namna ya kuchagua hekima.

a.       Hekima ya kweli inapatikana kwa kumcha Mungu – Mithali 1:7 “Kumcha Bwana ni chanzo cha maarifa, Bali wapumbavu hudharau hekima na adabu”.

b.      Uko umuhimu wa kumuomba Mungu hekima – Yakobo 1:5-6  Lakini mtu wa kwenu akipungukiwa na hekima, na aombe dua kwa Mungu, awapaye wote, kwa ukarimu, wala hakemei; naye atapewa.Ila na aombe kwa imani, pasipo shaka yo yote; maana mwenye shaka ni kama wimbi la bahari lililochukuliwa na upepo, na kupeperushwa huku na huku.”

2Nyakati 1:7-12 “Usiku ule Mungu akamtokea Sulemani, akamwambia, Omba utakalo nikupe. Sulemani akamwambia Mungu, Umemfanyia baba yangu Daudi fadhili kuu, nawe umenimilikisha mimi badala yake. Basi sasa, Ee Bwana Mungu, na limyakinie baba yangu Daudi neno lako; maana umenitawaza niwe mfalme juu ya watu wengi kama mavumbi ya nchi. Basi sasa nipe hekima na maarifa, nijue kutoka na kuingia mbele ya watu hawa; kwa kuwa ni nani awezaye kuwahukumu watu wako hawa walio wengi? Naye Mungu akamwambia Sulemani, Kwa sababu neno hili lilikuwamo moyoni mwako, wala hukujitakia mali, wala utajiri, wala utukufu, wala maisha za wakuchukiao, wala hukujitakia maisha ya siku nyingi; bali umejitakia hekima na maarifa, upate kuwahukumu watu wangu, niliokutawaza juu yao; basi hekima na maarifa umepewa; nami nitakupa mali, na utajiri, na utukufu, kupita walivyokuwa navyo wafalme wote waliokuwa kabla yako, wala baada yako hapatakuwa na mtu atakayekuwa navyo.  

c.       Hekima ni ulinzi – ukiwa na hekima hakuna kitu kitaharibika kila kitu kitarahisishwa kama vile fedha ilivyo ulinzi hekima itatuhifadhi zaidi kuliko fedha, tutapunguza kuharibikiwa endapo tutachagua hekima, Hekima ni njema hekima ni bora.

 

Muhubiri 7:11-12 “Hekima ni njema, mfano wa urithi; Naam, nayo ni bora kwao walionao jua. Kwa maana hekima ni ulinzi, kama vile fedha ilivyo ulinzi; na ubora wa maarifa ni ya kwamba hekima humhifadhi yeye aliye nayo.”                

d.      Chagua Hekima – Mithali 8:4-11 “Enyi watu, nawaita ninyi; Na sauti yangu ni kwa wanadamu.Enyi wajinga, fahamuni werevu, Nanyi wapumbavu, mpate moyo wa kufahamu. Sikieni, maana nitasema yaliyo mazuri, Na kufumbua midomo yangu kutakuwa maadili. Maana kinywa changu kitasema kweli, Na uovu ni chukizo kwa midomo yangu. Maneno yote ya kinywa changu yana haki; Hapana hata neno lililopotoka au la ukaidi. Yote humwelea yule afahamuye, Yote huelekea mbele yao waliopata maarifa.Pokea mafundisho yangu, wala si fedha, Na maarifa kuliko dhahabu safi. Maana hekima ni bora kuliko marijani; Wala vyote vinavyotamanika havilingani nayo.”

Ni muhimu kujikumbusha tena ya kuwa kukosa hekima ni gharama kubwa sana, kwani kinyume cha kukosa hekima ni kuwa mpumbavu, kila unachokiona duniani hakiendi vizuri ni kwa sababu watu walifanya upumbavu, upumbavu ni gharama kubwa sana na umewagharimu wengi, majuto makubwa sana duniani yamechangiwa na upumbavu uliofanywa na watu, sisi kama watu wa Mungu tunapaswa kumuomba Mungu atupe akili, atupe hekima ili tusifanye upumbavu, ambao unaweza kuja kuyagharimu maisha yetu na maisha ya wengine, maandiko yanatutaka tutembee na wenye hekima nasi tutakuwa na hiyo hekima.

Mithali 13:20 “Enenda pamoja na wenye hekima, nawe utakuwa na hekima; Bali rafiki wa wapumbavu ataumia.”

Ni mwenye hekima gani ambaye unaweza kuambatana naye au kwenda naye naye atakuambukiza hekima? Kwa kawaida wenye hekima pia huishi maisha matakatifu na ni nani aliye mtakatifu ni Yesu Kristo ambaye yeye anaitwa Hekima yetu yeye ni mkuu kuliko Suleimani na ana hekima kuliko Sulemani.

1Wakorintho 1:20-24 “Yu wapi mwenye hekima? Yu wapi mwandishi? Yu wapi mlete hoja wa zamani hizi? Je! Mungu hakuifanya hekima ya dunia kuwa ni upumbavu? Kwa maana katika hekima ya Mungu, dunia isipopata kumjua Mungu kwa hekima yake, Mungu alipenda kuwaokoa waaminio kwa upuzi wa lile neno linalohubiriwa. Kwa sababu Wayahudi wanataka ishara, na Wayunani wanatafuta hekima;bali sisi tunamhubiri Kristo, aliyesulibiwa; kwa Wayahudi ni kikwazo, na kwa Wayunani ni upuzi; bali kwao waitwao, Wayahudi kwa Wayunani, ni Kristo, nguvu ya Mungu, na hekima ya Mungu.

Mathayo 12:41-42 “Watu wa Ninawi watasimama siku ya hukumu pamoja na watu wa kizazi hiki, nao watawahukumu kuwa wamekosa; kwa sababu wao walitubu kwa mahubiri ya Yona; na hapa yupo aliye mkuu kuliko Yona. Malkia wa kusini atasimama siku ya hukumu pamoja na watu wa kizazi hiki, naye atawahukumu kuwa wamekosa; kwa sababu yeye alikuja kutoka pande za mwisho za dunia ili asikie hekima ya Sulemani, na hapa yupo aliye mkuu kuliko Sulemani.”

Kwa kuwa Yesu ndiye hekima yetu natoa ushauri kama maandiko yasemavyo, mpokee Yesu aliye hekima yetu ili kwamba uweze kuishi maisha ya neema na kujifunza kuwa kama yeye na kuishi maisha yasiyo na majuto chagua hekima mchague Yesu.Kumchagua Yesu ni Kuchagua hekima, na kuishi sawa na neno la Mungu ni kufuata njia ya Hekima, Bwana ampe neema kila mmoja wetu kuishi na kuenenda kwa hekima katika jina la Yesu Kristo ameen.  

Rev. Innocent Samuel Kamote.

Mkuu wa wajenzi mwenye hekima.