Jumapili, 19 Oktoba 2025

Na tazama, pazia la hekalu likapasuka!


Mathayo 27:50-54 “Naye Yesu akiisha kupaza sauti tena kwa nguvu, akaitoa roho yake. Na tazama, pazia la hekalu likapasuka vipande viwili toka juu hata chini; nchi ikatetemeka; miamba ikapasuka; makaburi yakafunuka; ikainuka miili mingi ya watakatifu waliolala; nao wakiisha kutoka makaburini mwao, baada ya kufufuka kwake, wakauingia mji mtakatifu, wakawatokea wengi. Basi yule akida, na hao waliokuwa pamoja naye wakimlinda Yesu, walipoliona tetemeko la nchi na mambo yaliyofanyika, wakaogopa sana, wakisema, Hakika huyu alikuwa Mwana wa Mungu.”




Utangulizi:

Mojawapo ya matukio makubwa ya kutisha na kushangaza yaliyoambatana na kifo cha Bwana wetu Yesu Kristo pale Msalabani ni pamoja na tukio la kupasuka kwa pazia la hekalu, tukio hili lina tupa ishara madhubuti juu ya umuhimu wa kifo cha Yesu Kristo na nguvu ya upatanisho iliyofanywa na kifo chake kwa wanadamu wote wakiwemo Wayahudi pia, Njia ya kuufikia uwepo wa Mungu ilikuwa sio rahisi wakati wa agano la kale na ni watu wachache sana waliokuwa na ruhusa ya kuukaribia uwepo wa Mungu. Pazia kubwa zito lilitenganisha mahali patakatifu sana palipokuwa na kiti cha rehema na uwepo wa watu wa kawaida hivyo kuwanyima watu fursa ya kukutana na Mungu bila mtu wa kuingilia kati. Pazia hili lilitengenezwa kwa maelekezo ya Mungu kwa Musa, likizuia eneo la Sanduku.

Kutoka 26:30-33 “Nawe utaisimamisha hiyo maskani sawasawa na mfano wake ulioonyeshwa mlimani. Nawe fanya pazia la nyuzi za rangi ya samawi, na za rangi ya zambarau, na za rangi nyekundu, na nguo za kitani nzuri zenye kusokotwa, litafumwa na kutiwa makerubi, kazi ya fundi stadi; kisha litungike katika nguzo nne za mti wa mshita zilizofunikwa dhahabu, vifungo vyake vitakuwa vya dhahabu, katika matako ya fedha manne. Nawe tungika lile pazia chini ya vile vifungo, nawe lete lile sanduku la ushuhuda na kulitia humo nyuma ya pazia; na lile pazia litawagawanyia kati ya patakatifu, na mahali patakatifu sana.”

Leo tutachukua muda kiasi kujifunza umuhimu wa pazia hili kupasuka wakati wa kifo cha Yesu Kristo na maana yake kubwa sana kwetu ambayo kimsingi inatupa tiketi ya kuuendea uwepo wa Mungu na kuufurahia ushirika na Mungu bila kupata madhara ya aina yoyote na bila ya kupitia kwa mtu yeyote, tutajifunza somo hili, Na tazama, Pazia la hekalu likapasuka kwa kuzingatia vipengele vikuu vitatu vifuatavyo:-


·         Kazi ya Pazia la hekalu.

·         Na tazama pazia la hekalu likapasuka.

·         Faida za kupasuka kwa pazia la hekalu.


Kazi ya pazia la Hekalu!

Pazia la Hekalu ilikuwa ni nguo maalumu iliyotengenezwa kwa nyuzi za kitani zilizofumwa kwa ustadi kwa rangi mchangayiko wa aina tatu, rangi ya samawi, yaani mbingu, rangi ya zambarau na nyekundu, Pazia hili lilikuwa na ukubwa kwa maana ya urefu wa futi sitini (Sawa na mita 18) na upana wa futi 30 (sawa na mita 9) na unene wake ulikuwa kati ya inchi 4 mpaka sita yaani kati ya sentimita 10-15. Aidha lilifumwa pia likiwa na picha ya makerubi mfano wa ulinzi kwaajili ya patakatifu pa patakatifu, Pazia hili lilikuwa na kazi ya kupafunika au kutenganisha mahali patakatifu na patakatifu sana. Pazia hili lilitengenezwa kwa ustadi kufuata maelekezo yaliyotolewa na Mungu.

Kutoka 36:35-38 “Kisha akafanya hilo pazia la nyuzi za rangi ya samawi, na za rangi ya zambarau, na nyekundu, na kitani nzuri zilizosokotwa; akatia na makerubi kazi ya fundi stadi, ndivyo alivyofanya. Naye akafanya kwa ajili yake nguzo nne za mti wa mshita, akazifunika dhahabu; na kulabu zake zilikuwa za dhahabu; naye akasubu kwa ajili yake matako manne ya fedha. Kisha akafanya pazia la sitara kwa ajili ya mlango wa Hema, la nguo ya rangi ya samawi, na ya rangi ya zambarau, na nyekundu, na nguo ya kitani nzuri ya kusokotwa, kazi ya mwenye kutia taraza, na nguzo zake tano pamoja na kulabu zake; naye akavifunika dhahabu vichwa vyake na vifungo vyake; na matako yake matano yalikuwa ya shaba.”

Kazi kubwa ya Pazia hili ilikuwa ni kutenganisha mahali patakatifu na patakatifu sana, hekalu lilikuwa na sehemu kubwa tatu, Patakatifu sana au patakatifu pa patakatifu mahali ambapo lilikaa sanduku la agano la Bwana, na patakatifu mahali ambapo palikuwa na madhabahu ya dhahabu ya kufukizia uvumba, taa ya vinara saba na meza ya mikate ya wonyesho, eneo hili kuhani aliingia kwaajili ya kufukiza uvumba, kila siku na kisha eneo la tatu ulikuwa ni uwa wa kawaida ambapo Wayahudi walikaa, na Mataifa wasio Wayahudi walikaa mbali zaidi katika uwa wa wamataifa. Pazia lilitenganisha mahali lilipokuwepo sanduku la agano ambalo juu yake kulikuwa na kiti cha rehema,  mahali hapa kuhani mkuu aliingia mara moja tu kwa mwaka kufanya upatanisho kwa watu na Mungu, siku ya upatanisho tena akiwa amejitakasa kweli kweli (siku saba maalumu kabla ya kuingia katika ibada hiyo), Pazia hili ni alama ikiwa na fundisho kuwa Mungu ni MTAKATIFU SANA na sio rahisi mwanadamu wa kawaida kumsogelea bila kupata madhara, Pazia hili zito lilikuwa ni katazo kuwa huwezi kuufikia uwepo wa Mungu wala kuona ukawa salama, Kuhani mkuu mwenyewe aliingia hapa mara moja kwa mwaka wala si pasipo damu tena siku ya upatanisho (Yom Kippur) kutoa dhabihu ya dhambi kwaajili yake, familia yake na watu wa taifa zima! Kinyume chake kifo kingehusika.

Kutoka 30:10 “Naye Haruni atafanya upatanisho juu ya pembe zake mara moja kila mwaka; kwa damu ya ile sadaka ya dhambi ya kufanya upatanisho, mara moja kila mwaka ataifanyia upatanisho, katika vizazi vyenu vyote; ni takatifu sana kwa BWANA.”

Waebrania 9:1-9 “Basi hata agano la kwanza lilikuwa na kawaida za ibada, na patakatifu pake, pa kidunia. Maana hema ilitengenezwa, ile ya kwanza, mlimokuwa na kinara cha taa, na meza, na mikate ya Wonyesho; ndipo palipoitwa, Patakatifu. Na nyuma ya pazia la pili, ile hema iitwayo Patakatifu pa patakatifu, yenye chetezo cha dhahabu, na sanduku la agano lililofunikwa kwa dhahabu pande zote, mlimokuwa na kopo la dhahabu lenye ile mana, na ile fimbo ya Haruni iliyochipuka, na vile vibao vya agano; na juu yake makerubi ya utukufu, yakikitia kivuli kiti cha rehema; basi hatuna nafasi sasa ya kueleza habari za vitu hivi kimoja kimoja. Basi, vitu hivi vikiisha kutengenezwa hivyo, makuhani huingia katika hema hiyo ya kwanza daima, wakiyatimiza mambo ya ibada. Lakini katika hema hiyo ya pili kuhani mkuu huingia peke yake, mara moja kila mwaka; wala si pasipo damu, atoayo kwa ajili ya nafsi yake na kwa dhambi za kutokujua za hao watu. Roho Mtakatifu akionyesha neno hili, ya kwamba njia ya kupaingia patakatifu ilikuwa haijadhihirishwa bado, hapo hema ya kwanza ilipokuwa ingali ikisimama; ambayo ndiyo mfano wa wakati huu uliopo sasa; wakati huo sadaka na dhabihu zinatolewa, zisizoweza kwa jinsi ya dhambi kumkamilisha mtu aabuduye,”

Kwa sababu hii watu wa kawaida hawakuweza kabisa kupakaribia mahali hapa, kwani hata kuhani alivalishwa kengele (njuga) maalumu kiunoni na mguuni na kufungwa kamba maalumu ili kama atapigwa na Mungu na kufa wamvute nje, watu wengine wote, wangekuwa nje mbali wakiwa wametengwa mbali na mahali hapo patakatifu sana kwaajili ya dhambi na matakwa ya kisheria, hivyo pazia lilikuwa linawakilisha ugumu wa kuufikia uwepo wa Mungu, Pazia lilikuwa linawakumbusha wakati wote kuwa Mungu ni MTAKATIFU SANA na sisi wengine wote hatustahili, dhambi ilikuwa imetufarakanisha mbali na Mungu na hakuna jitihada yoyote ya kibinadamu inayoweza kutuunganisha, utaratibu wote huu ulikuwa pia unafundisha ya kwamba tunahitaji mtu wa kutupatanisha na Mungu, hakuna mwanadamu yeyote aliruhusiwa kupita kwenye pazia hili, maovu ya mwanadamu yalimfarikisha na Mungu.

Isaya 59:1-2 “Tazama, mkono wa Bwana haukupunguka, hata usiweze kuokoa wala sikio lake si zito, hata lisiweze kusikia; lakini maovu yenu yamewafarikisha ninyi na Mungu wenu, na dhambi zenu zimeuficha uso wake msiuone, hata hataki kusikia.”             

 

Na tazama pazia la hekalu likapasuka.

Katika namna ya kushangaza sana na isiyoweza kubuniwa kibinadamu Neno la Mungu katika agano jipya linatufahamisha katika injili zifafanazo zote kuwa pazia hili lililokuwa na unene wa nchi 4-6 hivi kwa njia ya muujiza mkubwa usiokuwa wa kibinadamu mara Yesu alipokata roho na kufa msalabani pazia hili la hekalu lilipasuka katikati vipande viwili kutoka juu hata chini! Muujiza huu usiokuwa wa kawaida ulirekodiwa katika injili zote tatu zifananazo.

Mathayo 27:50-51. “Naye Yesu akiisha kupaza sauti tena kwa nguvu, akaitoa roho yake. Na tazama, pazia la hekalu likapasuka vipande viwili toka juu hata chini; nchi ikatetemeka; miamba ikapasuka;”

Marko 15:37-38 “Naye Yesu akatoa sauti kuu, akakata roho. Pazia la hekalu likapasuka vipande viwili toka juu hata chini.”

Luka 23:44-45 “Hapo ilikuwa yapata saa sita, kukawa giza juu ya nchi yote hata saa kenda, jua limepungua nuru yake; pazia la hekalu likapasuka katikati.”

Kwa nini tukio hili linakuwa la muhimu kiasi hiki mpaka kila mtume anarekodi habari hii, kwa ujumla hili sio jambo dogo, lina kitu cha muhimu cha kutufundisha, Mwandishi wa kitabu cha Waebrania anaeleza kwamba sababu kubwa ni kuwa Yesu Kristo mwana wa Mungu alifanyika Mwana kondoo mkamilifu, aliyejitoa mwenyewe kama sadaka ya kudumu ya milele na kwa damu yake kuwa mpatanishi kati ya Mungu na wanadamu, Mwandishi anafafanua kuwa lile pazia linawakilisha mwili wa Yesu Kristo, kwa hiyo wakati mwili ule unasulubiwa kwa ajili ya dhambi zetu, Kristo anafanyika kuwa mpatanishi kati ya Mungu na wanadamu na hivyo hatuhitaji tena kuhani wa kuingia katika kiti cha rehema kwaajili yetu, na ukuta uliotutenganisha na Mungu umebomolewa, kusulubiwa kwa Yesu Kristo kumeleta uponyaji mkubwa sana kwetu wa kimwili na kiroho, na hatuhitaji tena mtu awaye yote ajifanye “dalali” wa kiroho, au ajifanye kuwa yeye  anaweza kutupatanisha na Mungu ni ukweli ulio wazi kuwa mpatanishi ni mmoja tu. Yesu Kristo!

Waebrania 10:19-21 “Basi, ndugu, kwa kuwa tuna ujasiri wa kupaingia patakatifu kwa damu ya Yesu, njia ile aliyotuanzia iliyo mpya, iliyo hai, ipitayo katika pazia, yaani, mwili wake; na kuwa na kuhani mkuu juu ya nyumba ya Mungu;”

Isaya 53:2-5 “Maana alikua mbele zake kama mche mwororo, Na kama mzizi katika nchi kavu; Yeye hana umbo wala uzuri; Na tumwonapo hana uzuri hata tumtamani. Alidharauliwa na kukataliwa na watu; Mtu wa huzuni nyingi, ajuaye sikitiko; Na kama mtu ambaye watu humficha nyuso zao, Alidharauliwa wala hatukumhesabu kuwa kitu. Hakika ameyachukua masikitiko yetu, Amejitwika huzuni zetu; Lakini tulimdhania ya kuwa amepigwa, Amepigwa na Mungu, na kuteswa. Bali alijeruhiwa kwa makosa yetu, Alichubuliwa kwa maovu yetu; Adhabu ya amani yetu ilikuwa juu yake, Na kwa kupigwa kwake sisi tumepona.”

1Timotheo 2:5-6 “Kwa sababu Mungu ni mmoja, na mpatanishi kati ya Mungu na wanadamu ni mmoja, Mwanadamu Kristo Yesu; ambaye alijitoa mwenyewe kuwa ukombozi kwa ajili ya wote, utakaoshuhudiwa kwa majira yake.

Waebrania 4:14-16 “Basi, iwapo tunaye kuhani mkuu aliyeingia katika mbingu, Yesu, Mwana wa Mungu, na tuyashike sana maungamo yetu. Kwa kuwa hamna kuhani mkuu asiyeweza kuchukuana nasi katika mambo yetu ya udhaifu; bali yeye alijaribiwa sawasawa na sisi katika mambo yote, bila kufanya dhambi. Basi na tukikaribie kiti cha neema kwa ujasiri, ili tupewe rehema, na kupata neema ya kutusaidia wakati wa mahitaji.”            

1Petro 2:9-10 “Bali ninyi ni mzao mteule, ukuhani wa kifalme, taifa takatifu, watu wa milki ya Mungu, mpate kuzitangaza fadhili zake yeye aliyewaita mtoke gizani mkaingie katika nuru yake ya ajabu; ninyi mliokuwa kwanza si taifa, bali sasa ni taifa la Mungu; mliokuwa hamkupata rehema, bali sasa mmepata rehema.”

1Wakorintho 6:19 “Au hamjui ya kuwa mwili wenu ni hekalu la Roho Mtakatifu aliye ndani yenu, mliyepewa na Mungu? Wala ninyi si mali yenu wenyewe;”      

 

Faida za kupasuka kwa pazia la hekalu

Kupasuka kwa Pazia la hekalu kunatupa faida lukuki ambazo muda usingeliweza kutosha kuelezea yote lakini njia ya kumuendea Mungu na kufanya ushirika naye leo imekuwa wazi kwa kila aaminiye, kutoka kokote kule duniani!

-          Tunaweza kumuendea Mungu kwa maombi na kuzungumza naye moja kwa moja bila dalali huku tukiwa na uhakika kuwa Mungu anatusikia  Wafilipi 4:6-7 “Msijisumbue kwa neno lo lote; bali katika kila neno kwa kusali na kuomba, pamoja na kushukuru, haja zenu na zijulikane na Mungu. Na amani ya Mungu, ipitayo akili zote, itawahifadhi mioyo yenu na nia zenu katika Kristo Yesu.”

 

-          Tunaweza kumuendea kwa ibada na kumuabudu kwa kumsifu na kumshukuru tukiwa na uhakika kuwa yeye ni Bwana Mungu wetu kwani tuna uwezo wa kuingia malangoni mwake Zaburi 100:4-5 “Ingieni malangoni mwake kwa kushukuru; Nyuani mwake kwa kusifu; Mshukuruni, lihimidini jina lake; Kwa kuwa Bwana ndiye mwema; Rehema zake ni za milele; Na uaminifu wake vizazi na vizazi.”

 

-          Tunaweza kulifurahia neno lake ambalo kimsingi zamani ni makuhani pekee ndio waliokuwa na uwezo wa kulisoma na kulifafanua kwa watu, Neno la Mungu sasa ni kwaajili ya kila mtu na linaeleweka kwa kila amtafutaye Mungu

 

2Timotheo 3:16-17 “Kila andiko, lenye pumzi ya Mungu, lafaa kwa mafundisho, na kwa kuwaonya watu makosa yao, na kwa kuwaongoza, na kwa kuwaadibisha katika haki; ili mtu wa Mungu awe kamili, amekamilishwa apate kutenda kila tendo jema.”

 

-          Tunaweza kuufurahia uwepo wa Mungu pamoja na wengine kwani kila tunapokutana na kukusanyika kwa jina lake yeye naye anaungana nasi na kuwa kati kati yetu.

 

Mathayo 18:18-20 “Amin, nawaambieni, yo yote mtakayoyafunga duniani yatakuwa yamefungwa mbinguni; na yo yote mtakayoyafungua duniani yatakuwa yamefunguliwa mbinguni. Tena nawaambia, ya kwamba wawili wenu watakapopatana duniani katika jambo lo lote watakaloliomba, watafanyiwa na Baba yangu aliye mbinguni. Kwa kuwa walipo wawili watatu wamekusanyika kwa jina langu, nami nipo papo hapo katikati yao.”

 

-          Tunaweza kuziungama dhambi zetu wenyewe moja kwa moja na Mungu akatusamehe bila kupitia kwa kuhani wa kibinadamu kama ilivyo katika baadhi ya dini ambapo makuhani hutaka kuwatawala wanadamu na kuwanyanyasa kisaikolojia kwa sababu wanataka kusikiliza dhambi zao, au wanafanya kazi ya upelelezi

 

1Yohana 1:8-9 “Tukisema kwamba hatuna dhambi, twajidanganya wenyewe, wala kweli haimo mwetu. Tukiziungama dhambi zetu, Yeye ni mwaminifu na wa haki hata atuondolee dhambi zetu, na kutusafisha na udhalimu wote.”            

 

Kupasuka kwa pazia la hekalu ni tukio la kusangaza sana na si la kihistoria tu bali ni kazi kubwa ya Mungu yenye kumaanisha kuwa Mungu anatoa mwaliko kwa kila mmoja kuukaribia uwepo wake haijalishi umetoka katika historia gani,  na wa kabila gani, Mungu sasa haishi nyuma ya pazia wala hafikiwi kupitia mtu, kuhani au dalali, lakini kupitia Bwana wetu Yesu Kristo mlango ulio wazi umefunguliwa kwa jamii nzima ya aina binadamu duniani kuwa huru na kuufikia uwepo wa Mungu, hakuna wa kujidai katikati yetu badala yake tunasaidiana na kujengana huku tukitiana moyo kwamba leo uiamini kazi  yake Bwana aliyoifanya msalabani kwamba imefungua njia kwaajili yako na yangu na Wayahudi wote duniani kokote waliko kwamba Mungu yuko tayari kukutana na kila mtu anayemjia katika jina la Yesu Kristo Mwana wa Mungu aliye hai Amen

               

Na. Rev. Innocent Samuel Kamote

 

Mkuu wa wajenzi mwenye Hekima!

Jumapili, 12 Oktoba 2025

Maumivu yako, maumivu yake!


Isaya 63:7-9 “Nitautaja wema wa Bwana, sifa za Bwana kwa yote aliyotukirimia Bwana; na wingi wa wema wake kwa nyumba ya Israeli, aliowakirimia kwa rehema zake, na kwa wingi wa wema wake. Maana alisema, Hakika ndio watu wangu hawa, wana wasio na hila; akawa Mwokozi wao.Katika mateso yao yote yeye aliteswa, na malaika wa uso wake akawaokoa; kwa mapenzi yake, na huruma zake, aliwakomboa mwenyewe; akawainua, akawachukua siku zote za kale.”

Utangulizi:

Tuwapo duniani wanadamu wote tunakutana na maumivu ya aina mbalimbali katika maisha, maumivu haya yanaweza yasilingane lakini kila mmoja anaweza kuhisi maumivu kwa jinsi yake, ziko nyakati maisha yanakuwa magumu, ziko nyakati tunaumia moyo, ziko nyakati tunalia machozi, ziko nyakati matumaini yanavunjika, ziko nyakati roho zinauma, kwa ujumla kunakuwa na maswali mengi sana hususani wakati tunapopitia maumivu haya, moyoni unaweza kuhisi kuwa labda Muumba naye angehisi maumivu haya, tunajiuliza anasikia na anaumia kama ninavyoumia? Mungu wetu anajali kweli? Neno la Mungu linaonyesha ya kuwa Mungu sio tu kuwa anayaona mateso yetu lakini pia anaumia pamoja nasi kama baba anavyowahurumia watoto wake ndivyo Mungu wetu anavyotuhurumia Maumivu yako ni maumivu yake!

Zaburi 103:11-14 “Maana mbingu zilivyoinuka juu ya nchi, Kadiri ile ile rehema zake ni kuu kwa wamchao. Kama mashariki ilivyo mbali na magharibi, Ndivyo alivyoweka dhambi zetu mbali nasi. Kama vile baba awahurumiavyo watoto wake, Ndivyo Bwana anavyowahurumia wamchao. Kwa maana Yeye anatujua umbo letu, Na kukumbuka ya kuwa sisi tu mavumbi.”

Mungu anatupenda mno, anaweza kuyatumia maumivu yetu kutimiza makusudi yake fulani fulani katika maisha yetu, lakini hata hivyo yeye hafurahii maumivu yetu na anapatwa na uchungu ule ule unaotupata sisi wakati wa maumivu yetu, anashiriki machozi yetu na anakaa nasi wakati wa mambo magumu na kutukomboa kuhakikisha usalama wetu na furaha yetu inakuwa kamilifu, Leo basi tutachukua muda kujifunza somo hili “Maumivu yako maumivu yake” kwa kuzingatia yafuatayo:-

·         Maana ya maumivu yako maumivu yake.

·         Mifano ya watu ambao Mungu alioshughulika na maumivu yao.

·         Maumivu yako maumivu yake.


Maana ya maumivu yako maumivu yake.

Usemi maumivu yako maumivu yake unatokana na maelezo ya unabii wa Isaya katika mstari wetu wa msingi tuliousoma ambao unaashiria kuwa, Mungu anaguswa sana na maumivu yetu, na ya kuwa anateseka pamoja na wanadamu wanaoteseka anasikia uchungu kama wanavyosikia uchungu, anahisi maumivu kama wanavyohisi maumivu, anaumia pale watoto wake wanapoumia, na Analia pale watoto wake wanapolia hii ndio maana kubwa tunayoipata katika mstari wa Msingi kutoka ktk

Isaya 63:9 “Katika mateso yao yote yeye aliteswa, na malaika wa uso wake akawaokoa; kwa mapenzi yake, na huruma zake, aliwakomboa mwenyewe; akawainua, akawachukua siku zote za kale.”

Neno katika mateso yao yote yeye aliteswa, Neno aliteswa katika lugha ya Kiebrania linasomeka kama “tsar tsar” ambalo katika kiingereza ni sawa na neno “Affliction” kwa hiyo katika kiingereza maneno Katika mateso yao yote yeye aliteswa yanasomeka “in all their affliction he was afflicted” neno hili ni sawa na kusema “Maadui zao wakawa maadui zake” au “Maumivu yao yakawa maumivu yake” au “Maumivu yako maumivu yake” au “Katika taabu zao alitaabika”hii maana yake ni kuwa Mungu anajua maumivu yako, anashiriki taabu zako na mashinikizo yako, anasikia uchungu wako kama mtu awaye yote mwenye huruma anavyohisi uchungu wa maumivu yako, wakati wote kama baba zetu wa duniani wanaposikia uchungu kwa habari ya maumivu ya watoto wao, Mungu wetu wa Mbinguni ambaye ni Baba anaguswa zaidi na maumivu yetu kuliko wanadamu ambao ni waovu, maandiko yanaonyesha ya kuwa Mungu ni Baba anayejali watoto wake kuliko, zaidi ya baba zetu wa duniani, ikiwa wao wanaumia kwaajili yetu, Mungu yeye Maumivu yako, ni maumivu yake!

Luka 11:11-13 “Maana ni yupi kwenu aliye baba, ambaye mwanawe akimwomba mkate, atampa jiwe au samaki, badala ya samaki atampa nyoka? Au akimwomba yai, atampa nge? Basi, ikiwa ninyi mlio waovu mnajua kuwapa watoto wenu vipawa vyema, je! Baba aliye mbinguni hatazidi sana kuwapa Roho Mtakatifu hao wamwombao?       

Mifano ya watu ambao Mungu alioshughulika na maumivu yao.

Biblia imejaa mifano mingi inayoonyesha jinsi ambavyo Mungu hakuwahi kuvumilia maumivu ya watu wake kwa sababu zozote zile, aliyajua maumivu, hofu na changamoto walizokuwa wanazipitia watu wake, alifahamu mashinikizo yao katika maisha na katika hekima yake na huruma zake aliweza kuwajali na kushughulikia kwa haraka, changamoto hizo kabla hawajamezwa kwa huzuni.

1.       Hajiri – Aliteswa na Sara Bibi yake kiutawala alimuamuru Abrahamu kumtupa na kumfukuzilia mbali majazi huko jangwani, Hajiri alikimbilia jangwani akiwa na mwanae ambaye alikuwa anakaribia kufa kwa kiu ya maji, walianza kulia katika jangwa, alimweka mtoto chini na kukimbilia mbali ili asimuone mtoto akifa, akalia kwa uchungu Mungu aliguswa na mateso na kilio cha mtoto na mama yake na akaleta ufumbuzi katika maisha yao

Mwanzo 21:14-19 “Ibrahimu akaamka asubuhi na mapema akatwaa mkate na kiriba cha maji, akampa Hajiri akimtwika begani pake, na kijana, akamruhusu; naye akatoka, akapotea katika jangwa la Beer-sheba. Yale maji yakaisha katika kiriba, akamlaza kijana chini ya kijiti kimoja.  Akaenda akakaa akimkabili, mbali naye kadiri ya mtupo wa mshale; maana alisema, Nisimwone kijana akifa; naye akakaa akimkabili, akapaza sauti yake, akalia. Mungu akasikia sauti ya kijana. Malaika wa Mungu akamwita Hajiri kutoka mbinguni, akamwambia, Una nini, Hajiri? Usiogope, maana Mungu amesikia sauti ya kijana huko aliko. Ondoka, ukamwinue kijana, ukamshike mkononi mwako, kwa kuwa nitamfanya kuwa taifa kubwa. Mungu akamfumbua macho, naye akaona kisima cha maji; akaenda akakijaza kiriba maji, akamnywesha kijana.”

2.       Israel Utumwani – Wote tunafahamu kuwa Israel walipata mikandamizo mingi na kuonewa na wasimamizi wao huko jangwani, hali ilikuwa mbaya kiasi ambacho Mungu alilazimika kuingilia kati kwaajili ya wokovu, ni ukweli ulio wazi kuwa Maumivu yao yalikuwa magumu na waliugua na kuumwa na shinikizo lile la utumwa usio wa kiungwana Maumivu yao yakawa  maumivu yake Mungu ambaye kimsingi aliguswa na kushuka akipanga wokovu wao

Kutoka 3:7-10 “BWANA akasema, Hakika nimeyaona mateso ya watu wangu walioko Misri, nami nimekisikia kilio chao kwa sababu ya wasimamizi wao; maana nayajua maumivu yao; nami nimeshuka ili niwaokoe na mikono ya Wamisri, niwapandishe kutoka nchi ile, hata nchi njema, kisha pana; nchi ijaayo maziwa na asali; hata mahali pa Mkanaani, na Mhiti, na Mwamori, na Mperizi, na Mhivi, na Myebusi. Basi, tazama, kilio cha wana wa Israeli kimenifikilia; tena nimeyaona hayo mateso ambayo Wamisri wanawatesa. Haya, basi, nitakutuma sasa kwa Farao, ili upate kuwatoa watu wangu, hao wana wa Israeli, katika Misri.”

3.       Mjane – Huyu mwanamke huko katika mji wa Naini alikuwa mjane, lakini licha ya kuwa mjane alikuwa na mwane mmoja kijana wa pekee, Neno la Mungu halisemi kulikuwa na mazingira gani kijana huyu alikufa na watu wa mji walitoka kwenda mazikoni, Yesu alipomuona mama huyu alimuhurumia maumivu yake yakawa maumivu ya Kristo, na akisukumwa na upendo wake na maumivu ya huruma zake Yesu alimfufua kijana yule mara!

Luka 7:11-15 “Baadaye kidogo alikwenda mpaka mji mmoja uitwao Naini, na wanafunzi wake walifuatana naye pamoja na mkutano mkubwa. Na alipolikaribia lango la mji, hapo palikuwa na maiti anachukuliwa nje, ni mwana pekee wa mamaye ambaye ni mjane, na watu wa mjini wengi walikuwa pamoja naye. Bwana alipomwona alimwonea huruma, akamwambia, Usilie. Akakaribia, akaligusa jeneza; wale waliokuwa wakilichukua wakasimama. Akasema, Kijana, nakuambia, Inuka. Yule maiti akainuka, akaketi, akaanza kusema. Akampa mama yake.”

4.       Lazaro – Alikuwa rafiki wa Yesu Kristo pamoja na dada zake Martha na Mariamu, Lazaro aliugua na baadaye akafa, Yesu alihudhuria msiba huu akiwa Mungu katika mwili aliguswa sana na maumivu ya dada zake Lazaro, ambao walilia wakiwa wamekata tamaa ya uhai, wakitarajia kuwa uwezekano wa kufufuka kwa Lazaro ni labda katika siku ya mwisho lakini akisukumwa na huruma maumivu yao yakawa maumivu yake Yesu akafanya tukio akamfufua

Yohana 11: 32-35 “Basi Mariamu alipofika pale alipokuwapo Yesu, na kumwona, alianguka miguuni pake, akamwambia, Bwana, kama ungalikuwapo hapa, ndugu yangu hangalikufa. Basi Yesu alipomwona analia, na wale Wayahudi waliofuatana naye wanalia, aliugua rohoni, akafadhaika roho yake, akasema, Mmemweka wapi? Wakamwambia, Bwana, njoo utazame. Yesu akalia machozi.”

Yohana 11:43-44 “Naye akiisha kusema hayo, akalia kwa sauti kuu, Lazaro, njoo huku nje. Akatoka nje yule aliyekufa, amefungwa sanda miguuni na mikononi, na uso wake amefungwa leso. Naye Yesu akawaambia, Mfungueni, mkamwache aende zake.”

Maumivu yako maumivu yake.

Tunajifunza kupitia neno la Mungu la msingi na mifano iliyopo katika maandiko ya kwamba Mungu wetu huwa anajishughulisha sana na mambo yetu na kwa sababu hiyo pia ni muhimu kufahamu kuwa maumivu yetu ni maumivu yake, kwa sababu hiyo hatakuacha ujaribiwe kupita uwezavyo, yuko tayari kabisa kutoa mapumziko kwa wote wanaaonewa na kukandamizwa na Shetani kwa sababu zozote zile. Usifikri hata kidogo kuwa tuna Mungu asiyejali, Maumivu yako ni maumivu yake!

1Petro 5:6-7 “Basi nyenyekeeni chini ya mkono wa Mungu ulio hodari, ili awakweze kwa wakati wake; huku mkimtwika yeye fadhaa zenu zote, kwa maana yeye hujishughulisha sana kwa mambo yenu.”

Mathayo 11:28 “Njoni kwangu, ninyi nyote msumbukao na wenye kulemewa na mizigo, nami nitawapumzisha.”

Mathayo 8:16-17 “Hata kulipokuwa jioni, wakamletea wengi wenye pepo; akawatoa pepo kwa neno lake, akawaponya wote waliokuwa hawawezi, ili litimie lile neno lililonenwa na nabii Isaya, akisema, Mwenyewe aliutwaa udhaifu wetu, Na kuyachukua magonjwa yetu.”            

Ni muhimu kwa sababu hiyo kukumbuka kuwa maumivu yako ni maumivu yake, Maumivu yako si dalili ya kuwa Mungu amekutupa bali ni njia ya kuthibitisha ya kuwa yuko pamoja nawe na anakujali sana, wakati wewe unalia kumbuka Mungu analia pamoja nawe, Mungu anayabeba maumivu yako kuliko yanavyobebwa na mwanasaikolojia yeyote yule, na sio hivyo tu yeye atakupa nguvu na kukuwezesha kwa msaada wa Roho wake Mtakatifu, kilio chako wakati wowote kinaweza kugeuka kuwa mbegu ya furaha na mafanikio yako, uchungu wako unatambuliwa na Mungu kwa hiyo kama alivyosema katika mateso yako yote yeye anateseka pamoja nawe kwa hiyo leo ishi ukifahamu ya kwamba maumivu yako ni maumivu yake, ole wake anayekuumiza anamuumiza Mungu, ole wake anayekulaani anamlaani Mungu, ole wake anayekugusa anamgusa Mungu.

Zekaria 2:8-10 “Kwa maana Bwana wa majeshi asema hivi, Ili nitafute utukufu amenituma kwa mataifa wale waliowateka ninyi; maana yeye awagusaye ninyi aigusa mboni ya jicho lake. Kwa maana, tazama, nitatikisa mkono wangu juu yao, nao watakuwa mateka ya hao waliowatumikia; nanyi mtajua ya kuwa Bwana wa majeshi amenituma. Imba, ufurahi, Ee binti Sayuni; maana, tazama, ninakuja, nami nitakaa kati yako, asema Bwana.”

Na. Rev. Innocent Samuel Kamote

Mkuu wa wajenzi mwenye Hekima!

Jumapili, 5 Oktoba 2025

Namjua anayeishika kesho!


Mathayo 6:31-34 “Msisumbuke, basi, mkisema, Tule nini? Au Tunywe nini? Au Tuvae nini? Kwa maana hayo yote Mataifa huyatafuta; kwa sababu Baba yenu wa mbinguni anajua ya kuwa mnahitaji hayo yote. Bali utafuteni kwanza ufalme wake, na haki yake; na hayo yote mtazidishiwa. Basi msisumbukie ya kesho; kwa kuwa kesho itajisumbukia yenyewe. Yatosha kwa siku maovu yake.”



Utangulizi:

Mojawapo ya tatizo kubwa la kiroho na kisaokolojia linalowakumba wanadamu ni pamoja na tatizo la kuogopa kesho au wakati ujao, tatizo la kuhofia kuhusu kesho au wakati ujao kisakolojia linaitwa “Chronophobia” au “time anxiety”  hofu ya wakati hususani wakati ujao ambayo kitaalamu inafafanuliwa kama “a type of anxiety that involves  worrying about tomorrow or future”  yaani ni aina ya msongo wa mawazo unaohusisha kuogopa au hofu kuhusu kesho au wakati ujao,  Neno Chronophobia ni muunganiko wa maneno mawili ya kiyunani “Chronos” yaani muda na “phobos” yaani hofu kwa hiyo wanadamu wengi wanasumbuliwa na hofu kubwa sana kuhusu itakuwaje kesho, katika Afrika wanawake wengi huongoza kwa hofu hii na ndio maana wengi huogopa kufiwa na waume zao na utawasikia wakisema kuna leo na kesho hali itakuwaje? Na wakati mwingine watu huogopa kuwa huenda kuna jambo baya litawatokea na watu wengi wanaogopa magumu, wengine huogopa muda kwa kufungwa gerezani, masikini huogopa kwamba kesho itakuwaje, matajiri huogopa kufilisika, wenye vyeo huogopa kuviachia, wafanya biashara huogopa hasara, Wengine huogopa muda kwa kufikiri kuwa wamekawia katika maisha, Tatizo la hofu linaweza kuwako katika pembe nyingi,  Ingawa tatizo hili linaweza kuwa la kawaida lakini kuna wanadamu wengine tatizo hili huwa kubwa zaidi kwao na linaweza kufikia hatua likaathiri Imani yao na ni kwa sababu hii Neno la Mungu linamtaka kila mmoja wetu kutokuogopa kuhusu kesho au wakati ujao na badala yake kumtegemea Mungu.

Mathayo 6:34 “Basi msisumbukie ya kesho; kwa kuwa kesho itajisumbukia yenyewe. Yatosha kwa siku maovu yake.”

Kwa nini neno la Mungu linatuonya kutokuogopa kesho? Hii ni kwa sababu Mungu ndiye anayeishika kesho, kesho yako na wakati wako ujao uko mikononi mwa Mungu na ukilitambua hilo huwezi kuogopa lolote, Kwa msingi huu basi leo tutachukua muda kujifunza kwa kina na mapana na marefu juu ya somo hili “Namjua anayeishika kesho” kwa kuzingatia vipengele vitatu vifuatavyo:-


·         Hofu ya wanadamu kuhusu kesho.

·         Neno la Mungu linasemaje kuhusu kesho.

·         Namjua anayeishika kesho.


Hofu ya wanadamu kuhusu kesho.

Mathayo 6:25-34 “Kwa sababu hiyo nawaambieni, Msisumbukie maisha yenu, mle nini au mnywe nini; wala miili yenu, mvae nini. Maisha je! Si zaidi ya chakula, na mwili zaidi ya mavazi? Waangalieni ndege wa angani, ya kwamba hawapandi, wala hawavuni, wala hawakusanyi ghalani; na Baba yenu wa mbinguni huwalisha hao. Ninyi je! Si bora kupita hao? Ni yupi kwenu ambaye akijisumbua aweza kujiongeza kimo chake hata mkono mmoja? Na mavazi, ya nini kuyasumbukia? Fikirini maua ya mashamba, jinsi yameavyo; hayafanyi kazi, wala hayasokoti nami nawaambia, ya kwamba hata Sulemani katika fahari yake yote hakuvikwa vizuri kama mojawapo la hayo. Basi, ikiwa Mungu huyavika hivi majani ya kondeni, yaliyopo leo, na kesho hutupwa kalibuni, je! Hatazidi sana kuwavika ninyi, enyi wa imani haba? Msisumbuke, basi, mkisema, Tule nini? Au Tunywe nini? Au Tuvae nini? Kwa maana hayo yote Mataifa huyatafuta; kwa sababu Baba yenu wa mbinguni anajua ya kuwa mnahitaji hayo yote. Bali utafuteni kwanza ufalme wake, na haki yake; na hayo yote mtazidishiwa. Basi msisumbukie ya kesho; kwa kuwa kesho itajisumbukia yenyewe. Yatosha kwa siku maovu yake.”

Katika hutuba yake ya mlimani Mwalimu wetu mkuu na mwokozi wa maisha yetu Yesu Kristo hakuacha kuzungumzia swala zima la hofu ya wanadamu kuhusu kesho, wanadamu wengi masikini kwa matajiri wote wanakabiliwa na hofu kuwa itakuwaje kesho au maisha ya baadaye, hofu hii inaweza ikawa sio tu kwa mahitaji ya kawaida nitakula nini na nitavaa nini, lakini inaweza kuwa zaidi ya hapo, itakuwaje nikifiwa na mume, itakuwaje nikifukuzwa kazi, itakuwaje nikifilisika, itakuwaje nikidaiwa kodi, itakuwaje nikiachwa! Itakuwaje nikiugua? Itakuwaje nikishindwa uchaguzi, itakuwaje nikifeli, nini kitatokea, itakuwaje uchumi ukiyumba? Na kadhalika hofu hii ni tatizo kubwa la kiroho na kisaikolojia na Mungu analijua vema, anajua kuwa hofu hizi zinaweza kumpelekea mtu akakosa Amani, akapoteza usingizi, na hatimaye akapoteza Imani na matumaini na Ndio maana Yesu aliwafundisha wanafunzi wake kwamba hawapaswi kuogopa kuhusu kesho kwa sababu Baba wa mbinguni anajua mahitaji yetu na ndiye anayeishika kesho!.

Neno la Mungu linasemaje kuhusu kesho.

Neno la Mungu linatufundisha ya kuwa ni Mungu ndiye mwenye uwezo wa kudhibiti kesho ya kila mmoja wetu, na hakuna mwanadamu ambaye anaweza kujisumbua kuhusu kesho yake na akafanikiwa bila neema na kibali cha Mungu, hofu yako wasiwasi wako na hata maandalizi yako hayawezi kukuhakikishia kesho iliyo salama na kamili bila Mungu, kwa sababu kesho haiko katika mikono ya mwanadamu bali iko katika mikono ya Mungu mwenyewe, wako watu ambao walijisumbua sana kuhusu kesho na neno la Mungu likawatumia kama mifano ya kutuonya kuwa huwezi kufanya kitu kuhusu kesho na ukajithibitishia usalama bila ya Mungu! Kesho iko kwenye mapenzi ya Mungu! Mungu ndiye anayeishika kesho ili mwanadamu asiwe na kiburi, Tancredo Neves alikuwa mgombea urais wa Brazili mwaka 1985 wakati wa kampeni zake alisema nikipata kura 500,000 tu kutoka kwenye chama changu hakutakuwa na wa kuzuia nisiwe Rais hata Mungu hataweza kunizuia, Kwa kweli alipata kura hizo na akashinda uchaguzi, lakini aliugua ghafla na utumbo ulijikunja akafariki siku moja kabla ya kuapishwa kuwa raisi Tarehe 21/4/1985. Lazima kila mmoja kwa unyenyekevu akubali kuwa kesho iko mikononi mwa Mungu na sio mikononi mwa mwanadamu.

Yakobo 4:13-15 “Haya basi, ninyi msemao, Leo au kesho tutaingia katika mji fulani na kukaa humo mwaka mzima, na kufanya biashara na kupata faida; walakini hamjui yatakayokuwako kesho. Uzima wenu ni nini? Maana ninyi ni mvuke uonekanao kwa kitambo, kisha hutoweka. Badala ya kusema, Bwana akipenda, tutakuwa hai na kufanya hivi au hivi.”

Luka 12:15-20 “Akawaambia, Angalieni, jilindeni na choyo, maana uzima wa mtu haumo katika wingi wa vitu vyake alivyo navyo. Akawaambia mithali, akisema, Shamba la mtu mmoja tajiri lilikuwa limezaa sana; akaanza kuwaza moyoni mwake, akisema, Nifanyeje? Maana sina pa kuyaweka akiba mavuno yangu. Akasema, Nitafanya hivi; nitazivunja ghala zangu, nijenge nyingine kubwa zaidi, na humo nitaweka nafaka yangu yote na vitu vyangu. Kisha, nitajiambia, Ee nafsi yangu, una vitu vyema vingi ulivyojiwekea akiba kwa miaka mingi; pumzika basi, ule, unywe, ufurahi. Lakini Mungu akamwambia, Mpumbavu wewe, usiku huu wa leo wanataka roho yako! Na vitu ulivyojiwekea tayari vitakuwa vya nani?               

Maandiko yanatuonya wazi kuwa hakuna mwanadamu anayeweza kudai kwa sababu zozote zile kwamba anaweza kuwa na uhakika wa kesho, na hata hivyo hatupaswi kuiogopa kesho pia, lakini kesho iko katika mikono ya Mungu na kwa sababu hiyo neno la Mungu linatuonya kuiacha hofu ya kesho katika mikono ya Mungu, badala yake tunatiwa moyo kumuamini Mungu na kumtegemea yeye kwaajili ya mahitaji yetu ikiwepo kesho yetu,  Neno la Mungu halitutii moyo kuogopa kuhusu kesho kwaajili ya mahitaji yetu, wala halituhakikishii kuwa tunaweza kutengeneza usalama wetu wa kesho kwa kujilimbikizia ua kujiwekea akiba au kwa kutafuta sana kunakoambatana na hofu ya kesho na pia hakuna mwanadamu awaye yote wa ngazi yoyote ile anayeweza kujithibitishia kuwa na kesho iliyo njema nje ya uweza na mamlaka ya Mungu Mwenyewe. Kwa sababu hiyo hatupaswi kujivuna au kujisifia lolote kuhusu kesho!

Mithali 27:1-2 “Usijisifu kwa ajili ya kesho; Kwa maana hujui yatakayozaliwa na siku moja. Mwingine na akusifu wala si kinywa chako mwenyewe; Mtu mgeni wala si midomo yako wewe.”

Neno la Mungu linaonyesha wazi kuwa mwenye kesho ni Mungu tu, siku moja tu inaweza kuzaa jambo na likabadilisha kila kitu katika maisha yetu, kwa sababu hiyo hatuna budi kuishi kwa unyenyekevu na kwa kumtegemea Mungu pake yake, hatupaswi kuiogopa kesho kama tunamwamini Mungu na wala hatupaswi kujihami kuhusu kesho kama iko mikononi mwa Mungu hii maana yake ni nini? Maana yake ni kuwa Mungu ndiye anayeishika kesho na ukimjua yeye hutaweza kuishi maisha ya hofu ya aina yoyote ile, ukiwa na uhakika kuwa kesho yako iko kwake!

Namjua anayeishika kesho.

Ni muhimu kufahamu kuwa hakuna hofu wala woga utakaokutawala endapo tu utagundua kuwa ni Mungu ndiye anayeishikilia kesho yako, Mungu anaweza kubadilisha mambo kwa usiku mmoja tu, ukitambua kuwa ni Mungu ndiye anayeishikilia kesho yako hakuna mwanadamu atakayekutisha wala kukutetemesha kuhusu yajayo, kesho yako haiko katika mikono ya wanadamu, iko katika mikono ya Mungu, ukimjua yeye anayeshika kesho hautaogopa mabadiliko ya aina yoyote ile, utamtegemea yeye ambaye ni ngome iliyo imara  naye hatakuangusha, Mwandishi wa Zaburi hakuwahi kuogopa mabadiliko yoyote yale kwa sababu alikuwa anamjua Mungu na kutambua ya kuwa ndiye anayeshikilia kila kitu kwa hiyo lolote litokee haliwezi kututisha kwa sababu yeye Mungu ndiye mwenye kesho yake!

Zaburi 46:1-7 “Mungu kwetu sisi ni kimbilio na nguvu, Msaada utakaoonekana tele wakati wa mateso. Kwa hiyo hatutaogopa ijapobadilika nchi, Ijapotetemeka milima moyoni mwa bahari. Maji yake yajapovuma na kuumuka, Ijapopepesuka milima kwa kiburi chake. Kuna mto, vijito vyake vyaufurahisha mji wa Mungu, Patakatifu pa maskani zake Aliye juu. Mungu yu katikati yake hautatetemeshwa; Mungu atausaidia asubuhi na mapema. Mataifa yalighadhibika, falme zikataharuki; Alitoa sauti yake, nchi ikayeyuka. Bwana wa majeshi yu pamoja nasi, Mungu wa Yakobo ni ngome yetu.”

Mungu wetu ni Mungu asiyebadilika, Yeye ni Yeye yule jana leo na hata milele, Yu hai, na bado anaendelea kubarikia watu wake, anaendelea kulinda watu wake, anakomboa watu wake, bado ni mtawala wa mbingu na nchi majira na nyakati, ziko mkononi mwake, hajawahi kupoteza nguvu zake wala uwezo wake Yeye bado ni Bwana Mungu aliyeziumba mbingu na nchi na bahari na vyote vilivyomo, Ndiye aliyeigawa bahari ya Shamu, akamzika Farao na majeshi yake, akawalisha watu wake kwa mana, akawanywesha maji kutoka katika mwamba, akawapigania dhidi ya adui zao, akatimiza ahadi zake kwa kuwapa nchi ya Mkanaani, nguvu zake hazijawahi kupungua, alimfufua Lazaro, alimtoa Petro na Paulo na Sila gerezani, hakuna nguvu inaweza kupingana naye, Yeye ndiye anayeishika kesho, kesho yako haiko kwa waganga wa kienyeji, kesho yako haiko kwa bosi wako, kesho yako haiko kwa wenye mamlaka au cheo, kesho yako haiko kwa wachawi, kesho yako haiko kwa wapiga ramli kesho yako inashikwa na Mungu aliye hai, muumba wa mbingu na nchi, uaminifu wake unazidi kizazi hata kizazi na yeye anatuwazia mema na yeye habadiliki ni Yeye Yule jana leo na hata milele, Hakuna mtu anayeweza kuichafua kesho yako, hakuna mtu anaweza kuizibia kesho yako, kesho yako iko katika mikono ya Mungu, ukimjua anayeishika kesho yako hutaogopa, hakuna wa kukurudisha nyuma, tunaweza tusijue lolote kuhusu kesho, lakini tunaweza kumjua anayeishika kesho! Naye ni mwenye nguvu!

Kama Mungu ndiye anayeishika kesho yako maana yake unaweza kumuamini yeye kuhusu kesho yako na kutokuogopa wakati ujao ukijua ya kuwa anatuwazia mema na ana mpango mzuri kwaajili yako:-

Yeremia 29:11 “Maana nayajua mawazo ninayowawazia ninyi, asema Bwana, ni mawazo ya amani wala si ya mabaya, kuwapa ninyi tumaini siku zenu za mwisho.”

Kama Mungu ndiye anayeishika kesho yako maana yake hupawi kuogopa endapo unazingirwa na maadui pande zote na wanakukusudia mabaya hawawezi kutimiza mpango wao kwa sababu mpango wao sio mkuu kama wa yule anayeishika kesho:-

Zaburi 31:13-15 “Maana nimesikia masingizio ya wengi; Hofu ziko pande zote. Waliposhauriana juu yangu, Walifanya hila wauondoe uhai wangu. Lakini mimi nakutumaini Wewe, Bwana, Nimesema, Wewe ndiwe Mungu wangu. Nyakati zangu zimo mikononi mwako; Uniponye na adui zangu, nao wanaonifuatia.”

Kama Mungu ndiye anayeishika kesho yako maana yake ni yeye anayeweza kukulinda kwa nguvu zake na mkono wake kiasi kwamba hutakuwa na lolote la kuogopa, hutaogopa wachawi, hutaogopa Shetani, hutaogopa, laana, hutaogopa wanaoukutishia maisha Imani na tumaini litakuwa kubwa kwa Bwana Mungu wako na hutaogopa vita wala majeshi makubwa ya adui yajapojipanga kupigana nawe kwa sababu yuko anayeishika kesho yako!

Zaburi 27:1-5 “Bwana ni nuru yangu na wokovu wangu, Nimwogope nani? Bwana ni ngome ya uzima wangu, Nimhofu nani? Watenda mabaya waliponikaribia, Wanile nyama yangu, Watesi wangu na adui zangu, Walijikwaa wakaanguka. Jeshi lijapojipanga kupigana nami, Moyo wangu hautaogopa. Vita vijaponitokea, Hata hapo nitatumaini. Neno Moja nimelitaka kwa Bwana, Nalo ndilo nitakalolitafuta, Nikae nyumbani mwa Bwana Siku zote za maisha yangu, Niutazame uzuri wa Bwana, Na kutafakari hekaluni mwake. Mradi atanisitiri bandani mwake siku ya mabaya, Atanisitiri katika sitara ya hema yake, Na kuniinua juu ya mwamba.”

Kama Mungu ndiye anayeishika kesho yetu tunajengewa uhakika na matumaini ya kuwa anajishughulisha sana na mambo yetu, atakutana na mahiaji yetu, na tutaishi kwa kujiamini bila kuogopa tukijua ya kua kesho ni ya Baba mwenye upendo na rehema ataishughulikia, sina ada italipwa, sina chakula nitakula, sina nguo nitavaa, sina raha nitapewa, nina mizigo itapumzishwa, nina madeni yatalipwa, sioni njia ataniongoza, naona giza atakuwa nuru!

Kumbukumbu 8:11-16 “Jihadhari, usije ukamsahau Bwana, Mungu wako, kwa kutozishika amri zake, na hukumu zake, na sheria zake, ninazokuamuru leo. Angalia, utakapokuwa umekula na kushiba, na kujenga nyumba nzuri na kukaa ndani yake; na makundi yako ya ng'ombe na kondoo yatakapoongezeka, na fedha yako na dhahabu yako itakapoongezeka, na kila kitu ulicho nacho kitakapoongezeka; basi hapo moyo wako usiinuke, ukamsahau Bwana, Mungu wako, aliyekutoa katika nchi ya Misri, katika nyumba ya utumwa; aliyekuongoza katika jangwa lile kubwa lenye kitisho, lenye nyoka za moto na nge, nchi ya kiu isiyokuwa na maji; aliyekutolea maji katika mwamba mgumu, aliyekulisha jangwani kwa mana, wasiyoijua baba zako; apate kukutweza, apate kukujaribu, ili kukutendea mema mwisho wako.”

Kama Mungu ndiye anayeishika kesho yako, maana yake ni kuwa haitakuja utishike na kuweweseka kwa sababu yeye yuko siku zote, alikuwako tangu mwanzo, habadiliki, hageuki wala hana kigeugeu, wala kwake hakuna kubadilika badilika Yeye ni Yeye yule jana leo na hata milele  Waebrania 13:8 “Yesu Kristo ni yeye yule, jana na leo na hata milele.”

Yakobo 1:17 “Kila kutoa kuliko kwema, na kila kitolewacho kilicho kamili, hutoka juu, hushuka kwa Baba wa mianga; kwake hakuna kubadilika, wala kivuli cha kugeuka-geuka.”

Kama Mungu ndiye anayeishika kesho yetu basi ni wazi kuwa hakuna jambo lolote lile linaloweza kututenga na upendo wake, hakuna wa kutuhukumu, hakuna wa kututishia maisha, hakuna wa kututishia kuhusu kesho, hakuna wa kutupunguzia kitu, hakuna wa kutupokonya ushindi, hakuna wa kututisha kwa maana kesho iko mikononi mwake

Warumi 8:31-39 “Basi, tuseme nini juu ya hayo? Mungu akiwapo upande wetu, ni nani aliye juu yetu? Yeye asiyemwachilia Mwana wake mwenyewe, bali alimtoa kwa ajili yetu sisi sote, atakosaje kutukirimia na mambo yote pamoja naye? Ni nani atakayewashitaki wateule wa Mungu? Mungu ndiye mwenye kuwahesabia haki. Ni nani atakayewahukumia adhabu? Kristo Yesu ndiye aliyekufa; naam, na zaidi ya hayo, amefufuka katika wafu, naye yuko mkono wa kuume wa Mungu; tena ndiye anayetuombea. Ni nani atakayetutenga na upendo wa Kristo? Je! Ni dhiki au shida, au adha, au njaa, au uchi, au hatari, au upanga? Kama ilivyoandikwa, ya kwamba, Kwa ajili yako tunauawa mchana kutwa, Tumehesabiwa kuwa kama kondoo wa kuchinjwa. Lakini katika mambo hayo yote tunashinda, na zaidi ya kushinda, kwa yeye aliyetupenda. Kwa maana nimekwisha kujua hakika ya kwamba, wala mauti, wala uzima, wala malaika, wala wenye mamlaka, wala yaliyopo, wala yatakayokuwapo, wala wenye uwezo, wala yaliyo juu, wala yaliyo chini, wala kiumbe kinginecho chote hakitaweza kututenga na upendo wa Mungu ulio katika Kristo Yesu Bwana wetu.”

Na. Rev. Innocent Samuel Kamote

Mkuu wa wajenzi mwenye Hekima!

Jumapili, 28 Septemba 2025

Kuishi zaidi ya maneno!


Zaburi 109:1-3. “Ee Mungu wa sifa zangu, usinyamaze, Kwa maana wamenifumbulia kinywa; Kinywa cha mtu asiye haki, cha hila, Wamesema nami kwa ulimi wa uongo.  Naam, Kwa maneno ya chuki wamenizunguka, Wamepigana nami bure.”




Utangulizi:

Wote tutakuwa tunafahamu nguvu kubwa iliyoko katika maneno, maneno yana nguvu!, yana nguvu kubwa kiasi cha kuweza kujenga, yana nguvu kubwa kiasi cha kuweza kubomoa, yana uwezo wa kuponya, yana uwezo wa kujeruhi, yana uwezo wa kutia moyo, yana uwezo wa kuvunja moyo, Neno la Mungu linasema kuwa maneno yana uwezo wa kuleta mauti au kuleta uzima unaona!

Mithali 18:20-21 “Tumbo la mtu litajazwa matunda ya kinywa chake; Atashiba mazao ya midomo yake. Mauti na uzima huwa katika uwezo wa ulimi; Na wao waupendao watakula matunda yake.”

Leo nataka tuzungumzie kile ambacho Roho Mtakatifu anataka nikizungumzie kwaajili ya watu wake anaotaka kuwasaidia na hii ni kuishi zaidi ya maneno hasi, Ujumbe huu ulinijia kwa lugha ya kiingereza “Beyond the negative words” lakini mimi nahudumia watu wanaozungumza Kiswahili, kwa hiyo nimeUita ujumbe huu Kuishi zaidi ya maneno!, Kila mtu aliyemwamini Mungu anapaswa kuishi zaidi ya maneno, hususani maneno hasi yaani yale yanayokuja kwetu kupitia Shetani na mawakala wake ambao wanatutupia maneno ili tuishi kwa mipaka, ili tukate tamaa, ili tuvunjike moyo, ili tushindwe, ili tuogope, ili tusiendelee, ili tutawalike, ili kutuonea na kutujeruhi, ili kuondoa ujasiri wetu, ili ususie na kadhalika, Roho Mtakatifu amenituma nikutie moyo kwamba unaweza kuishi zaidi ya maneno, na kuwa wako watakatifu waliotutangulia ambao kimsingi walishi zaidi ya maneno na wakapata ushindi na kusonga mbele katika maisha yao ya kawaida na ya kiroho Ishi zaidi ya maneno, Tutajifunza somo hili kuishi zaidi ya maneno kwa kuzingatia vipengele vitatu vifuatavyo:-

·         Maneno ya kuvunja moyo.

·         Wanadamu na maneno ya kuvunja moyo.

·         Kuishi zaidi ya maneno


Maneno ya kuvunja moyo.

Mojawapo ya namna na jinsi Shetani anavyowashambulia watu wa Mungu ni pamoja na kuwashambulia kwa maneno, hususani maneno ya kuvunja moyo, Shetani anaweza kuwatumia watu yaani mawakala wake, na wanaweza kuwa na sura yoyote ile, wanaweza kuwa ni waamini wenzako, waimbaji wenzako katika kwaya, watumishi wenzako, wakristo wenzako ndugu au watu wa karibu na wakati mwingine watu wa ulimwengu huu watakurushia maneno ya kukuvunja moyo, ili ujihoji kama unastahili, uwe na mashaka, uwe na wasiwasi hata kuhusu ahadi za Mungu, watakuhukumu, watakujaza woga na hofu, watashambulia imani yako, watakuvunja moyo, wataiba furaha yako. Shetani anaweza kutumia marafiki, maadui na jamii na wakati mwingine hata moyoni mwako unaweza ukajihukumu! Kwamba labda wewe sio bora sana, wewe sio mwema sana, labda wewe huwezi kufanikiwa, hutoboi, au Mungu amekuacha, maneno haya yatakushambulia kama mshale yakitafuta kukuvunja moyo na kukukatisha tamaa na unaweza hata kudhani kuwa labda wokovu kwako hauna maana au Mungu hana msaada kwako, Kristo Yesu alishambuliwa kwa maneno wakati akiwa msalabani katika hali ya mateso.

Luka 23:35-37 “Watu wakasimama wakitazama. Wale wakuu nao walikuwa wakimfanyia mzaha, wakisema, Aliokoa wengine; na ajiokoe mwenyewe, kama ndiye Kristo wa Mungu, mteule wake. Wale askari nao wakamfanyia dhihaka, wakimwendea na kumletea siki, huku wakisema, Kama wewe ndiwe mfalme wa Wayahudi, ujiokoe mwenyewe.”

Luka 23:38-39 “Na juu yake palikuwa na anwani; HUYU NDIYE MFALME WA WAYAHUDI. Na mmoja wa wale wahalifu waliotungikwa alimtukana, akisema, Je! Wewe si Kristo? Jiokoe nafsi yako na sisi.”

Mathayo 27:39-43 “Nao waliokuwa wakipita njiani wakamtukana, wakitikisa-tikisa vichwa vyao, wakisema, Ewe mwenye kulivunja hekalu na kulijenga kwa siku tatu, jiokoe nafsi yako; ukiwa ndiwe Mwana wa Mungu, shuka msalabani. Kadhalika na wale wakuu wa makuhani wakamdhihaki pamoja na waandishi na wazee, wakisema, Aliokoa wengine, hawezi kujiokoa mwenyewe. Yeye ni mfalme wa Israeli; na ashuke sasa msalabani, nasi tutamwamini. Amemtegemea Mungu; na amwokoe sasa, kama anamtaka; kwa maana alisema, Mimi ni Mwana wa Mungu.”

Neno la Mungu linaonya na kukemea, likitaka wanadamu wawe na matumizi mazuri ya ulimi yaani maneno kwani yanaweza kusababisha madhara makubwa sana, uharibifu wa aina nyingi sana duniani na hata vita kubwa duniani zilianza na ulimi tu, talaka, majungu makazini, kufukuzwa watu kazi, kuharibia wengine maisha kumesababishwa kwa kiwango kikubwa na ulimi, yaani maneno maneno yameumiza wengi, yameua wengi, yamefarakanisha wengi, yamechongea wengi na kuleta uharibifu katika maisha ya wengi kiroho, kiakili, kiuchumi, kisaikolojia na kadhalika.

Yakobo 3:5-6 “Vivyo hivyo ulimi nao ni kiungo kidogo, nao hujivuna majivuno makuu. Angalieni jinsi moto mdogo uwashavyo msitu mkubwa sana. Nao ulimi ni moto; ule ulimwengu wa uovu, ule ulimi, umewekwa katika viungo vyetu, nao ndio uutiao mwili wote unajisi, huuwasha moto mfulizo wa maumbile, nao huwashwa moto na jehanum.”             

Wanadamu na maneno ya kuvunja moyo

Hebu tuwe wakweli tu maneno ya kuvunja moyo ni sehemu ya maisha ya Mwanadamu, tunaishi katika ulimwengu uliooza na kuharibikwa kwa dhambi, kwa sababu hiyo aidha watu kwa kupenda au hata kwa kutokupenda, kwa kudhamiria au hata kwa kutokudhamiria, watapiga domo, watapiga umbeya, wanadamu ni wambeya wanadamu ni waongo wanadamu wana maneno yaliyojaa sumu, wanadamu wana maneno, wanadamu ni wazushi, watu wana maneno watu wanazungumza bhana maneno ya kuumiza, maneno ya kubomoa, maneno ya kukosesha watu wanasengenya, ukiwa mwema utasengenywa, ukiwa mbaya utasengenywa, vyovyote uwavyo kila mwanadamu anasemwa mahali fulani na wakati mwingine wanazungumza maneno yanayoumiza sana, wanazungumza maneno ya kuharibu, wanazungumza vitu vya kuharibu usalama wako, wanakuweka uchi, wanakuwekea mipaka, wanaharibu maisha, na wakati mwingine wanatumiwa wazi wazi na adui Shetani kuumiza na kukatisha tamaa wengine na hata waliookoka huingia katika mtego huu na hata sisi wenyewe tunaweza kujifikiri vibaya kama hatutaacha kujitazama katika mtazamo wa Mungu, kwa ujumla ndimi za wanadamu zimejaa sumu, yaani watu wana maneno yenye madhara na wanaweza kuzungumza bila kujifikiri, hawafikiri madhara, hawafikiri mauti wanatumiwa tu na yule shetani, ukitenda mema watasema, ukitenda mabaya watasema ni mawakala wa Shetani.

Zaburi 140:1-3. “Ee Bwana, uniokoe na mtu mbaya, Unihifadhi na mtu wa jeuri. Waliowaza mabaya mioyoni mwao, Kila siku huondokesha vita. Wamenoa ndimi zao kama nyoka, Sumu ya fira i chini ya midomo yao.”

Kwa hiyo utakubaliana nami kuwa maneno ya kukatisha tamaa ni sehemu ya maisha ya kila siku na ya kawaida katika ulimwengu huu wa watu wasio wakamilifu, Mwandishi wa Zaburi amewahi kulalamika kuwa wakati mwingine hata rafiki zetu wa karibu wanaweza kutunenea mabaya, watu tunaosali nao pamoja, marafiki na hata ndugu, yaani yeyote anaweza kutumiwa! Haijalishi ni nani!

Zaburi 55:12-14 “Kwa maana aliyetukana si adui; Kama ndivyo, ningevumilia. Aliyejitukuza juu yangu siye anichukiaye; Kama ndivyo, ningejificha asinione. Bali ni wewe, mtu mwenzangu, Rafiki yangu, niliyejuana nawe sana. Tulipeana shauri tamu; na kutembea Nyumbani mwa Mungu pamoja na mkutano.”

Warumi 3:10-14 “kama ilivyoandikwa, ya kwamba, Hakuna mwenye haki hata mmoja. Hakuna afahamuye; Hakuna amtafutaye Mungu. Wote wamepotoka, wameoza wote pia; Hakuna mtenda mema, la! Hata mmoja. Koo lao ni kaburi wazi, Kwa ndimi zao wametumia hila. Sumu ya fira i chini ya midomo yao.Vinywa vyao vimejaa laana na uchungu.”

Endapo hutajifunza na kuelewa kwa kina na mapana na marefu Neno la Mungu unaweza kusumbuka sana, lakini ukielewa kuwa tuko Duniani na Dunia imejaa wazushi na waongo na waharibifu na wasema vibaya na waumizaji hutaweza kuishi zaidi ya maneno “Beyond the negative words” Lakini ashukuriwe Mungu atupaye kushinda Roho Mtakatifu atatuwezesha kuishi zaidi ya maneno, Maneno ni aina ya vita, ambayo Shetani anaitumia, kama ilivyo katika ulimwengu wa kawaida mabondia na wapiganaji kabla ya kupigana huanza na tambo za maneno au propaganda hii ni vita ambayo watakatifu waliotutangulia waliifahamu na kujua namna na jinsi ya kuipigana, kwa nini Shetani hutumia vita vya maneno kuwashambulia watu wa Mungu hii ni kwa sababu:-

-          Unashambuliwa ili ujisahau kuwa wewe ni nani – anataka usahahu kuwa wewe ni chagua la Mungu na Mungu amekuumba kwa jinsi ya ajabu, amekuumba kwa kusudi na kwa ushindi na kukuita kwenye kusudi lake kwa sababu hiyo ni lazima Shetani akushambulie, akushitaki.

 

Zaburi 139:13-14Maana Wewe ndiwe uliyeniumba mtima wangu, Uliniunga tumboni mwa mama yangu, Nitakushukuru kwa kuwa nimeumbwa Kwa jinsi ya ajabu ya kutisha. Matendo yako ni ya ajabu, Na nafsi yangu yajua sana,”

 

1Petro 2:9-10 “Bali ninyi ni mzao mteule, ukuhani wa kifalme, taifa takatifu, watu wa milki ya Mungu, mpate kuzitangaza fadhili zake yeye aliyewaita mtoke gizani mkaingie katika nuru yake ya ajabu; ninyi mliokuwa kwanza si taifa, bali sasa ni taifa la Mungu; mliokuwa hamkupata rehema, bali sasa mmepata rehema.”

 

-          Unashambuliwa ili utoke katika kusudi la Mungu – Maneno yanaweza kukutia mashaka na kukufadhaisha ili ikiwezekana yakutoe katika mpango na mapenzi ya Mungu au kusudi ambalo kwalo Mungu amekuitia

 

Nehemia 4:1-3 “Lakini ikawa, Sanbalati aliposikia ya kwamba tulikuwa tukiujenga ukuta, akaghadhibika, akaingiwa na uchungu sana, akawadhihaki Wayahudi. Akanena mbele ya nduguze na mbele ya jeshi la Samaria, akisema, Wayahudi hawa wanyonge wanafanyaje? Je! Watajifanyizia boma? Watatoa dhabihu? Au watamaliza katika siku moja? Je! Watayafufua mawe katika chungu hizi za kifusi, nayo yameteketezwa kwa moto? Basi Tobia, Mwamoni, alikuwa karibu naye, akasema, Hata hiki wanachokijenga, angepanda mbweha, angeubomoa ukuta wao wa mawe.”              

 

-          Unashambuliwa kwaajili ya kuidhoofisha Imani – Maneno yanaweza kutumika kama njia ya kukuvunja moyo, ili ushindwe kulitimiza kusudi la Mungu kwa Imani na kurudi katika mashaka Israel walipokuwa wanakaribia kuingia katika inchi ya Kanaani wapelelezi kumi walitumiwa na shetani wakwavunja moyo watu kwa maneno yao na watu wakakubali kuvunjika moyo.

 

Hesabu 13:31-33Bali wale watu waliopanda pamoja naye wakasema, Hatuwezi kupanda tupigane na watu hawa; kwa maana wana nguvu kuliko sisi. Wakawaletea wana wa Israeli habari mbaya ya ile nchi waliyoipeleleza, wakasema, Ile nchi tuliyopita kati yake ili kuipeleleza, ni nchi inayowala watu wanaoikaa; na watu wote tuliowaona ndani yake ni watu warefu mno. Kisha, huko tuliwaona Wanefili, wana wa Anaki, waliotoka kwa hao Wanefili; tukajiona nafsi zetu kuwa kama mapanzi; nao ndivyo walivyotuona sisi.”

 

Hesabu 14:1-3 “Mkutano wote wakapaza sauti zao wakalia; watu wakatoka machozi usiku ule. Kisha wana wa Israeli wote wakamnung'unikia Musa na Haruni; mkutano wote wakawaambia, Ingekuwa heri kama tungalikufa katika nchi ya Misri, au, ingekuwa heri kama tungalikufa katika jangwa hili. Mbona Bwana anatuleta mpaka nchi hii ili tuanguke kwa upanga? Wake zetu na watoto wetu watakuwa mateka; je! Si afadhali turudi Misri?”                           

Kuishi zaidi ya maneno;

Ili kila mtu duniani awe na amani ya kweli na ushindi dhidi ya maneno ya kukatisha tamaa na kuumiza moyo tunayokuta nayo duniani basi inatulazimu kuishi zaidi ya maneno hasi, na ili uweze kuishi zaidi ya maneno unapaswa kuishi kwa kuliangalia Neno la Mungu linasema nini juu yako na sio kile watu wanachokisema, wewe na mimi sio matokeo ya kile watu wanasema wewe na mimi ni matokeo ya kile Mungu anachokisema Neno la Mungu lina nguvu kuliko nyundo ivunjayo mawe vipande vipande, Neno la Mungu ni moto mkali wenye nguvu ya kuumba!

Yeremia 23:28-29 “Nabii aliye na ndoto, na aseme ndoto yake; na yeye aliye na neno langu, na aseme neno langu kwa uaminifu. Makapi ni kitu gani kuliko ngano? Asema Bwana. Je! Neno langu si kama moto? Asema Bwana; na kama nyundo ivunjayo mawe vipande vipande?”

Watakatifu waliopata ushindi katika kila vita waliyokutana nayo ya maneno walijikita katika Neno la Mungu na ujuzi wao kuhusu Mungu, ukawafanya wawe washindi, wale walioogopa maneno walinywea lakini wale walioliangalia neno la Mungu na kile Mungu ameahidi hawakuogopa

a.       Daudi na Gloiath – Walipigana vita vya maneno kwanza kabla ya kuingia katika vita halisi, Goliathi aliogopewa sana sio tu kwa sababu ya ukubwa wake lakini pia kwa sababu ya maneno yake hasi ambayo yalitisha sana na watu wote wakaogopa na pia walimkimbia ilikuwa ni aibu kubwa sana. Lakini Daudi alifahamu namna ya kushughulika naye. Daudi alikutana na maneno mengi ya kukatisha tamaa lakini yeye aliishi zaidi ya maneno! Ona:-

 

1Samuel 17: 1-11 “Wakati huo Wafilisti walikusanya majeshi yao kwa vita, nao wakakusanyika huko Soko, ulio mji wa Yuda, wakatua kati ya Soko na Azeka, katika Efes-damimu. Naye Sauli na watu wa Israeli wakakusanyika, wakatua katika bonde la Ela, nao wakapanga vita juu ya hao Wafilisti.Wafilisti wakasimama juu ya mlima upande huu, na Waisraeli wakasimama juu ya mlima upande huu, napo palikuwa na hilo bonde katikati. Ndipo akatoka shujaa katika kambi ya Wafilisti, aliyeitwa Goliathi, wa Gathi, ambaye urefu wake ulikuwa mikono sita na shibiri moja. Alikuwa na chapeo ya shaba kichwani, tena amevaa darii ya shaba; na uzani wake ile darii ya shaba ulikuwa shekeli elfu tano za shaba. Tena amevaa mabamba ya shaba miguuni mwake, naye alikuwa na mkuki wa shaba kati ya mabega; yake. Na mti wa fumo lake ulikuwa kama mti wa mfumaji; na kichwa cha mkuki wake kilikuwa shekeli mia sita za chuma uzito wake; na mtu aliyemchukulia ngao yake akamtangulia. Naye akasimama, akawapigia kelele majeshi ya Israeli akawaambia, Mbona mmetoka kupanga vita? Je! Mimi si Mfilisti, na ninyi si watumishi wa Sauli? Jichagulieni mtu, akanishukie mimi. Kama akiweza kupigana nami na kuniua, sisi tutakuwa watumwa wenu; nami nikimshinda yeye na kumwua, ninyi mtakuwa watumwa wetu, na kututumikia. Yule Mfilisti akasema, Nayatukana leo majeshi ya Israeli; nipeni mtu tupigane. Basi Sauli na Israeli wote waliposikia maneno hayo ya Mfilisti, wakafadhaika na kuogopa sana.”

 

1Samuel 17:24-28 “Na watu wote wa Israeli walipomwona yule mtu wakakimbia, wakaogopa sana. Watu wa Israeli wakasema, Je! Mmemwona mtu huyu aliyepanda huko? Hakika ametokea ili awatukane Israeli; basi, itakuwa, mtu yule atakayemwua, mfalme atamtajirisha kwa utajiri mwingi, naye atamwoza binti yake, na kuifanya mbari ya baba yake kuwa huru katika Israeli. Daudi akaongea na watu waliosimama karibu, akisema, Je! Atafanyiwaje yeye atakayemwua Mfilisti huyo, na kuwaondolea Israeli aibu hii? Maana Mfilisti huyu asiyetahiriwa ni nani hata awatukane majeshi ya Mungu aliye hai? Nao watu wakamjibu vivyo hivyo, wakisema, Ndivyo atakavyofanyiwa mtu yule atakayemwua. Naye Eliabu, mkubwa wake, alisikia hapo alipoongea na watu; na hasira yake Eliabu ikawaka juu ya Daudi, akasema, Mbona wewe umeshuka hapa? Na kondoo wale wachache umemwachia nani kule nyikani? Mimi nakujua kiburi chako, na ubaya wa moyo wako; maana umeshuka ili upate kuvitazama vita.”

 

1Samuel 17:32-33 “Daudi akamwambia Sauli, Asizimie moyo mtu ye yote kwa ajili ya huyu; mimi mtumishi wako nitakwenda kupigana na Mfilisti huyu. Sauli akamwambia Daudi, Huwezi wewe kumwendea Mfilisti huyu upigane naye; maana wewe u kijana tu; na huyu ni mtu wa vita tangu ujana wake.”

 

1Samuel 17:37 “Daudi akasema, Bwana aliyeniokoa na makucha ya simba, na makucha ya dubu, ataniokoa na mkono wa Mfilisti huyu. Sauli akamwambia Daudi, Enenda, na Bwana atakuwa pamoja nawe.”

 

1Samuel 17:42-46Hata Mfilisti alipotazama huku na huku, akamwona Daudi akamdharau; kwa kuwa ni kijana tu mwekundu, tena ana sura nzuri. Mfilisti akamwambia Daudi, Je! Mimi ni mbwa hata umenijia kwa fimbo? Mfilisti akamlaani Daudi kwa miungu yake. Mfilisti akamwambia Daudi, Njoo huku kwangu; nyama yako nitawapa ndege wa angani na wanyama wa mwituni. Ndipo Daudi akamwambia yule Mfilisti, Wewe unanijia mimi na upanga, na fumo, na mkuki, bali mimi ninakujia wewe kwa jina la Bwana wa majeshi, Mungu wa majeshi ya Israeli uliowatukana.Siku hii ya leo Bwana atakuua mkononi mwangu, nami nitakupiga, na kukuondolea kichwa chako, nami leo nitawapa ndege wa angani na wanyama wa nchi mizoga ya majeshi ya Wafilisti, ili kwamba dunia nzima wajue ya kuwa yuko Mungu katika Israeli.”

 

Daudi ni mfano wa watu ambao hawakukubali kuishi kwa maneno ya kukatisha tamaa kama angeyasikiliza aibu kubwa ingelipata taifa zima la Israel, lakini aliishi zaidi ya maneno alimkiri Mungu mwenye nguvu aliyeweza kumuokoa yeye na wanyama wakali wakiwepo simba na dubu akitambua ya kuwa Mungu huyu na neno lake ana nguvu kuliko maneno na umbile la adui

 

b.      Hanna na Penina – Hana alipata maneno ya kuumiza na kukatisha tamaa kutoka kwa Penina kwa sababu Hana hakuwa na watoto, alichokozwa na kusemwa vibaya kwa maneno hasi Penina alifanya hivyo mwaka kwa mwaka mpaka Hana aliacha kula na kusikitishwa sana naye

 

1Samuel 1:6-7 “Ila mwenzake humchokoza sana, hata kumsikitisha, kwa sababu Bwana alikuwa amemfunga tumbo. Tena mumewe akafanya hivyo mwaka kwa mwaka, hapo yule mwanamke alipokwea kwenda nyumbani kwa Bwana, ndivyo yule alivyomchokoza; basi, kwa hiyo, yeye akalia, asile chakula.”

 

Hata pamoja na maneno ya kuumiza na kukatisha tamaa Hana alifamya uamuzi wa kuishi zaidi ya maneno yeye aliongeza kasi kwenye maombi na kumlilia Mungu na Mungu hakumuangusha kwani alimjibu na kumpa mtoto Samuel na watoto wengine, kinywa cha Hana kilizungumza lugha nyingine kwa furaha

 

1Samuel 2:1-10 “Naye Hana akaomba, akasema, Moyo wangu wamshangilia Bwana, Pembe yangu imetukuka katika Bwana, Kinywa changu kimepanuka juu ya adui zangu; Kwa kuwa naufurahia wokovu wako; Hakuna aliye mtakatifu kama Bwana; Kwa maana hakuna ye yote ila wewe, Wala hakuna mwamba kama Mungu wetu. Msizidi kunena kwa kutakabari hivyo; Majivuno yasitoke vinywani mwenu; Kwa kuwa Bwana ni Mungu wa maarifa, Na matendo hupimwa na yeye kwa mizani. Pinde zao mashujaa zimevunjika, Na hao waliojikwaa wamefungiwa nguvu. Walioshiba wamejikodisha ili kupata chakula, Na hao waliokuwa na njaa wamepata raha. Naam, huyo aliyekua tasa amezaa watoto saba, Na yeye aliye na wana wengi amedhoofika. Bwana huua, naye hufanya kuwa hai; Hushusha hata kuzimu, tena huleta juu. Bwana hufukarisha mtu, naye hutajirisha; Hushusha chini, tena huinua juu. Humwinua mnyonge kutoka mavumbini, Humpandisha mhitaji kutoka jaani, Ili awaketishe pamoja na wakuu, Wakakirithi kiti cha enzi cha utukufu; Kwa maana nguzo za dunia zina Bwana, Naye ameuweka ulimwengu juu yake. Yeye atailinda miguu ya watakatifu wake; Bali waovu watanyamazishwa gizani, Maana kwa nguvu hakuna atakayeshinda; Washindanao na Bwana watapondwa kabisa; Toka mbinguni yeye atawapigia radi; Bwana ataihukumu miisho ya dunia; Naye atampa mfalme wake nguvu, Na kuitukuza pembe ya masihi wake.”

 

Kaka zangu na dada zangu Mungu anatutaka tuishi zaidi maneno, hatuishi kwa sababu ya maneno ya watu tunaishi kwa sababu ya neno la Mungu, ushindi wa maisha yetu umefungwa katika neno la Mungu na sio katika maneno ya wanadamu sisi ni washindi na zaidi ya kushinda. Hakikisha katika maisha yako unajaa neno la Mungu ili kila neno utakaloshambuliwa uwe unajibu lake katika neno la Mungu Ni neno la Mungu tu litakaloulinda moyo wako na mashambulizi ya shetani, litaiweka sawa akili yako litakulinda na kukuhifadhi  maneno ya kukatisha tamaa hayatakuwa na nguvu kwa mtu aliyejaa neno la Mungu ushindi wako utakuwa kama Daudi dhidi ya Goliati na Hana dhidi ya Penina, au Nehemia na akina Sanbalati, jifiche katika neno la Mungu imba ahadi zake kumbuka hakuna silaha itakayofanyika juu yako ambayo itafanikiwa na kila ulimi utakaoinuka dhidi yako katika kuhukumu utauhukumu kuwa mkosa na huu ndio urithi wa watumishi wa Mungu!

 

Isaya 54:17 “Utathibitika katika haki; utakuwa mbali na kuonewa, kwa maana hutaogopa; na mbali na hofu, kwa maana haitakukaribia.Tazama, yamkini watakusanyana; lakini si kwa shauri langu. Watu wo wote watakaokusanyana juu yako wataanguka kwa ajili yako. Tazama, nimemwumba mhunzi avukutaye moto wa makaa, akatoa silaha kwa kazi yake; nami nimemwumba mharibu ili aharibu. Kila silaha itakayofanyika juu yako haitafanikiwa na kila ulimi utakaoinuka juu yako katika hukumu utauhukumu kuwa mkosa. Huu ndio urithi wa watumishi wa Bwana, na haki yao inayotoka kwangu mimi, asema Bwana.”

Na Rev. Innocent Samuel Kamote

Mkuu wa wajenzi mwenye Hekima