Jumapili, 18 Juni 2017

Nendeni Mkwamwambie Yule Mbweha!


Andiko La msingi: Luka 13:32 “Akawaambia, Nendeni, mkamwambie yule mbweha, Tazama, leo na kesho natoa pepo na kuponya wagonjwa, siku ya tatu nakamilika.”


Wengi wetu tutakuwa tunafahamu, jinsi Mafarisayo walivyokua wapinzani wakubwa sana wa Bwana Yesu katika huduma yake na kazi zake, Katika kifungu hicho hapo juu hatuna uhakika kama Mafarisayo walikuwa wametumwa na Herode kweli, au walitunga uongo wao wenyewe ili kumtoa Yesu katika KUSUDI kuu la kazi yake ambalo lilikuwa ni kuutangaza Ufalme wa Mbinguni. Tunasoma hivi katika Mukhtadha mzima wa habari hii:-…



Luka 13:31-33 “Saa ile ile Mafarisayo kadha wa kadha walimwendea, wakamwambia, Toka hapa, uende mahali pengine, kwa sababu Herode anataka kukuua.  Akawaambia, Nendeni, mkamwambie yule mbweha, Tazama, leo na kesho natoa pepo na kuponya wagonjwa, siku ya tatu nakamilika.  Pamoja na hayo imenipasa kushika njia yangu leo na kesho na kesho kutwa; kwa kuwa haimkini nabii aangamie nje ya Yerusalemu.”

Yesu alikuwa katika mipaka ya galilaya wakati huu, Mafarisayo walimjia wakijifanya kama wanaurafiki na Yesu na kuwa wanamtakia mema, wanataka kuokoa maisha yake wana uchungu na maisha yake, walijifanya wana habari hizi kutoka kwa Herode kwamba Herode anataka kukuua hivyo uondoke, Yesu alitaka kuwaonyesha Mafarisayo hawa kuwa kama wamekubali kuwa wajumbe wa Herode yeye anawarejesha tena kwa Herode, na anawatuma waende wapeleke taarifa hii maana wamekubali kutumiwa kama wambeya sasa wamweleze wazi Herode na Yesu anatumia neno gumu

Nendeni Mkamwambie yule Mbweha!
Mbweha ni kijimnyama dhaifu sana  na kioga ambacho kinafanana na Mbwa, ni vinjinyama vinavyoishi mwituni vina uwezo wa kubweka lakini ni vioga, viongo na vichafu na vimejaa hila,huwinda wanyama wengine ni mnyama asiye na Heshima wala umaarufu na ni mnyama anayedharauliwa sana!

Yesu Kristo aliifahamu sheria kuwa imeandikwa usimnenee mabaya mkuu wa watu wako, Hivyo Yesu kimsingi hakuwa anamtukana Herode au kumnenea mabaya, Lakini alimuita mbweha kwa sababu  Yesu alikuwa anatambua roho ya ukatili aliyokuwa nayo Herode alikuwa anafahamu jinsi Herode alivyosumbua wengi kwa ukatili wake, alitambua kuwa Herode alikuwa amepoteza umaarufu kwa wayahudi na tena alikuwa ni kibaraka tu wa warumi na Kaisari, alikuwa muoga na mwenye hila na aliyepoteza umaarufu kabisa, 

 Yesu alikuwa anajua kuwa Herode hataki yeye awepo katika mipaka yake, na hivyo anataka kumtisha ili Yesu akimbilie mji mwingine, Majibu ya Bwana Yesu yalikuwa ya kumuondoa wasiwasi huyu Mbweha kuhusu huduma anayoifanya,

 Yesu alikuwa anajua kusudi la kuwepo kwake na hata saa ya kufa kwake, alikuwa anajua kusudi la Mungu katika maisha yake na hivyo mbwembwe  za Herode hazikuwa tishio kwake, watu wengi walimuogopa Herode kama Simba lakini Yesu alimuona Herode kama mbweha tu, Hivyo Yesu alitaka kumhakikishia Herode kuwa Yeye yupo kwa mapenzi ya Mungu katika ardhi ya Mungu na kuwa anatimiza kazi ya baba yake tu, na kuwa haogopi lolote! Aidha katika wakati huu Yesu alikuwa amepata umaarufu mkubwa sana na watu wengi walikuwa wamemuamini na kwa vile Yesu ni wa ukoo wa Daudi watu wengi walikuwa wameanza kujenga imani ya kuwa Yesu ndiye mfalme ajaye na mwokozi wa Israel Yesu alitambua wazi kuwa Yeye hakuzaliwa kwa kusudi la kutawala serikali ya wakti ule, Yeye alikuwa amekuja kufanya kazi ya ukombozi wa Mwanadamu kwa kufa na kufufuka kwake na hivyo alitambua kusudi la kuweko kwake!

Natoa Pepo na Kuponya wagonjwa!
Aidha Yesu alimtangazia Herode kupitia wajumbe wake ukweli kuwa anaendelea kufanya kazi ya Mungu katika mipaka ya Herode na kuwa ataendelea kufanya kazi ya Mungu, Ni kama Yesu alikuwa anamwambia Herode kuwa Haogopi wala hana hofu yoyote ya njama za Herode, Badala yake naendelea kutimiza kusudi la Mungu kwa kuwa yuko ndani ya majira na saa ya Mungu na haogopi vitisho, aidha Herode hapaswi kuogopa kwa kuwa Yesu anafanya kazi ya Mungu kwa muda mfupi tu,
Yesu Kristo ni kama alikuwa alikuwa akimjibu Herode kuwa kutoa Pepo na kuponya wagonjwa na kuhubiri injili leo na kesho tu (Kwa maana ya muda mfupi tu) kulikuwa na maana ya kuwa hakuwa anavunja sheria, hakuna ubaya wowote ambao Yesu alikuwa akiutenda, kutoa pepo na kuponya wagonjwa kwa siku chache tu, na kuwa Yesu baadaye angeondoka katika Mipaka yake kwa wakati wa Mungu na sio wa Herode.

Siku ya tatu nakamilika
Yesu alikuwa akitoa Muda tu wa kinabii kuwa siku ya tatu anakamilika, hii haikuwa na maana ya siku tatu katika jimbo la Galilaya, hii ilikuwa na maana ya siku tatu katika mpango wa Mungu na Muda wa Mungu, Yesu alikuwa anafahamu kuwa hakuna wa kumuua wala wa kumuondoa mpaka Muda wa Mungu utakapowadia, Yesu alikuwa na ujuzi kuwa atakwenda Yerusalem na huko ndiko atakakofia na kufufuka na kurudi katika enzi yake Mbinguni.

Ndugu Momaji wangu Jambo lolote lile linalokuja katika maisha yako, kukutisha na kukudhoofisha na kukutia woga na kukuvunja moyo na kukukatisha tamaa ni MBWEHA!  

Kama unaifanya kazi ya Mungu wewe ni mtumishi au nabii mamlaka uliyo nayo kwa Mungu ni kubwa kuliko ya watawala wa kisiasa, timiza kusudi la kazi uliyoitiwa bila kuogopa vitisho
Ndoto yako na maono yake yasitishwe na mtu awaye yote.

Hatuishi duniani kwa kubahatisha wala hatutimizi kusudi la kuweko kwetu kijinga, Mungu ndiye alpha na omega, hatima ya maisha yetu haiku mikononi mwa mtu Fulani au kiongozi Fulani iko mikononi mwa Mungu.

Wachawi ni Mbweha tu hawana hatima ya maisha yetu, waganga ni mbweha tu, wambea ni mbweha tu, wazushi ni mbweha tu, wafitinini mbweah tu, Kaaa katika kusudi la Mungu mtu awaye yote asikutishe, Usiondoke katika kusudi lako la Utumishi, kusoma, kufanya biashara, wokovu, malengo na mipango yako muhimu, ndoa yako na kadhalika, Kumbuka lolote linalotaka kukutoa katika mpango wa Mungu ni Mbweha tu!

Ujumbe: Na Mkuu wa Wajenzi Mwenye Hekima
Rev. Innocent Kamote
kwa Mawasiliano, Maoni, ushauri na shukrani wasiliana nami:-
 
0718990796
0784394550
0626606608 SMS only
ikamote@yahoo.com

Hakuna maoni: