Jumatano, 16 Oktoba 2024

Kutoka Misri kwa ujeuri!


Kutoka 14:5-8 “Mfalme wa Misri aliambiwa ya kuwa wale watu wamekwisha kimbia; na moyo wa Farao, na mioyo ya watumishi wake, iligeuzwa iwe kinyume cha hao watu, nao wakasema, Ni nini jambo hili tulilotenda, kwa kuwaacha Waisraeli waende zao wasitutumikie tena? Akaandalia gari lake, akawachukua watu wake pamoja naye; tena akatwaa magari mia sita yaliyochaguliwa, na magari yote ya Wamisri, na maakida juu ya magari hayo yote. Na BWANA akaufanya moyo wake Farao mfalme wa Misri kuwa mgumu, naye akawafuata wana wa Israeli; kwa sababu wana wa Israeli walitoka kwa ujeuri.”

 



Utangulizi:

Leo tutachukua Muda kutafakari kwa kusudi la kujifunza na kupandisha imani zetu kwanini maandiko yanasema Israel walitioka Misri kwa ujeuri? Jambo ambalo lilimfanya Farao kubadili mawazo na kuamua kuwafuatilia wana wa Israel baada ya kikao cha Dharula cha baraza la mawaziri na majeshi yake, kujadili kuwa imekuwaje wakawaachia Israel waende zao? Na wasiwatutumikie tena? Uchumi wao utasimamaje bila watumwa? Kazi zote ngumu za uzalishaji mali zitafanywa na nani? Kwanini tunawaachia watumwa waende kwa uhuru hata bila kupigana nao? Au kutumia nguvu kuwarejesha? Baada ya hoja nzito mswada ulipitishwa kuwa ni lazima watu hao warejeshwe utumwani vinginevyo tutapata hasara kubwa sana!

Kutoka 14:5-10 “Mfalme wa Misri aliambiwa ya kuwa wale watu wamekwisha kimbia; na moyo wa Farao, na mioyo ya watumishi wake, iligeuzwa iwe kinyume cha hao watu, nao wakasema, Ni nini jambo hili tulilotenda, kwa kuwaacha Waisraeli waende zao wasitutumikie tena? Akaandalia gari lake, akawachukua watu wake pamoja naye; tena akatwaa magari mia sita yaliyochaguliwa, na magari yote ya Wamisri, na maakida juu ya magari hayo yote. Na BWANA akaufanya moyo wake Farao mfalme wa Misri kuwa mgumu, naye akawafuata wana wa Israeli; kwa sababu wana wa Israeli walitoka kwa ujeuri.Wamisri wakafuata nyuma yao, farasi zote na magari yote ya Farao, na askari zake wenye kupanda farasi, na jeshi lake, nao wakawapata hali wamepanga pale karibu na bahari, karibu na Pi-hahirothi, kukabili Baal-sefoni. Hata Farao alipokaribia, wana wa Israeli wakainua macho yao, na tazama, Wamisri wanakuja nyuma yao; wakaogopa sana; wana wa Israeli wakamlilia BWANA.”

Leo tunapojifunza somo hili Roho Mtakatifu ananiambia kuwa kuna watu watatoka kwa jeuri, wataondoka katika mateso yao kwa mkono ulionyooshwa wa Bwana, watafunguliwa vifungo vyao kwa nguvu na uweza wa Mungu wetu, watakombolewa kutoka katika mateso yao na maumivu yao na majonzi yao, na utumwa wa kila aina unaoyazinga maisha yao, na kila kitu chenye kusononesha maisha yako leo kitakuwa ndio mwisho wa utawala wake katika maisha yako nawe utaenda zako kwa jeuri, Nasema leo utatoka kwa ujeuri katika jina la Yesu Kristo mwana wa Mungu aliye hai haleluyaaa! Tutajifunza somo hili kutoka Misri kwa ujeuri kwa kuzingatia vipengele vikuu vitatu vifuatavyo:-


·         Maana ya kutoka kwa jeuri

·         Nani ni sababu ya Jeuri yetu

·         Kutoka Misri kwa ujeuri

 

Maana ya kutoka kwa jeuri

Kutoka 14:8 “Na BWANA akaufanya moyo wake Farao mfalme wa Misri kuwa mgumu, naye akawafuata wana wa Israeli; kwa sababu wana wa Israeli walitoka kwa ujeuri.”

Katika kifungu hiki cha maandiko tunajifunza namna na jinsi Mungu alivyoingilia kati swala zima la mateso ya watu wake waliokuwa wanateseka kule Misri, Mungu alikuwa amechoshwa na utawala katili wa Farao, asiyekuwa na shukurani ambaye aliwatumia watumishi wake na wasimamizi wake kuwatesa wana wa Israel na kuwaletea msiba mkubwa na mateso makubwa kiasi ambacho waliugua na kumlilia Mungu.

Kutoka 3:7-9 “BWANA akasema, Hakika nimeyaona mateso ya watu wangu walioko Misri, nami nimekisikia kilio chao kwa sababu ya wasimamizi wao; maana nayajua maumivu yao; nami nimeshuka ili niwaokoe na mikono ya Wamisri, niwapandishe kutoka nchi ile, hata nchi njema, kisha pana; nchi ijaayo maziwa na asali; hata mahali pa Mkanaani, na Mhiti, na Mwamori, na Mperizi, na Mhivi, na Myebusi. Basi, tazama, kilio cha wana wa Israeli kimenifikilia; tena nimeyaona hayo mateso ambayo Wamisri wanawatesa.”

Wote tunakumbuka namna Mungu alivyotekeleza mpango wake ambao mara kwa mara ulikuwa ukikataliwa na Farao vilevile kwa jeuri aliyokuwa nayo, akigoma kabisa kuwaachia wana wa Israel na kuwaongezea machungu na mateso makali zaidi huku akijaa kiburi na kujifanya hamtambui Bwana na kuwa watu hao wana kauli za uongo na ni wavivu hivyo akawakazia kazi ngumu zaidi.

Kutoka 5:1-9 “Hata baadaye, Musa na Haruni wakaenda wakamwambia Farao, wakasema, BWANA, Mungu wa Israeli, asema hivi, Wape watu wangu ruhusa waende, ili kunifanyia sikukuu jangwani.Farao akasema, BWANA ni nani, hata niisikilize sauti yake, na kuwapa Israeli ruhusa waende zao? Mimi simjui BWANA, wala sitawapa Israeli ruhusa waende zao. Wakasema, Mungu wa Waebrania amekutana nasi; twakuomba, tupe ruhusa twende safari ya siku tatu jangwani, tumtolee dhabihu BWANA, Mungu wetu; asije akatupiga kwa tauni, au kwa upanga. Mfalme wa Misri akawaambia Enyi Musa na Haruni, mbona mnawaachisha watu kazi zao? Enendeni zenu kwa mizigo yenu.Kisha Farao akasema, Tazameni, watu wa nchi sasa ni wengi, nanyi mnawapumzisha, wasichukue mizigo yao. Na siku ile ile Farao akawaamuru wasimamizi wa watu, na wanyapara wao, akisema, Msiwape watu tena majani ya kufanyia matofali, kama mlivyofanya tangu hapo; na waende wakatafute majani wenyewe. Lakini hesabu ya matofali waliyokuwa wakifanya tokea hapo, wawekeeni iyo hiyo, msiipunguze hata kidogo, kwa maana ni wavivu hao; kwa hiyo wanapiga kelele, wakisema, Tupe ruhusa twende kumtolea Mungu wetu dhabihu.Wapeni watu hao kazi nzito zaidi, waitaabikie; wala wasiangalie maneno ya uongo.”

Jambo hili liliwapa uchungu wana wa Israel zaidi, hali yao wakati wanadai uhuru wa ruhusa ilibadilika kuwa mbaya na chungu zaidi, Jambo lilopelekea sasa Mungu kuanza kumuadhibu Farao kwa mapigo mazito sana huku akiwapendelea wana wa Israel ambao walianza kupata faraja kwa kutokuguswa na mapigo mazito, mapigo yaliyendelea mpaka lilipofika pigo la kumi ambalo lilisababisha msiba mkubwa kuanzia kwa Farao mpaka kwa wanyama wao na watumwa wao wote kila mahali walifiwa na mzaliwa wa kwanza jambo lililopelekea kutoa ruhusa ya haraka haraka ili wana wa Israel waende zao wakamuabudu Mungu kwa uhuru na pasipo hofu! Mungu mwenye nguvu YHWH alijionyesha uwezo wake na kumtiisha mfalme mwenye kiburi awaachie watu wake ambao kimsingi nao waliondoka kwa mikogo sana waliondoka kwa furaha na walindoka Misri kwa ujeuri ni nini maana ya wana wa Israel kuondoka kwa Jeuri ambacho kimsingi kilimfanya Farao abadilishe maamuzi? Hilo ndilo jambo la msingi ambalo tunataka kujifunza kwa kila leo ili nasi tutoke kwa ujeuri katiika kila Nyanja ambayo ibilisi ameweka mkono wake! tuchunguze andiko hilo kwa kina tena !

Kutoka 14:8 “Na BWANA akaufanya moyo wake Farao mfalme wa Misri kuwa mgumu, naye akawafuata wana wa Israeli; kwa sababu wana wa Israeli walitoka kwa ujeuri.”

Farao aliwafuta tena wana wa Israel kwa kiburi kwa sababu wana wa Israel walitoka kwa ujeuri ni nini hasa maana ya ujeuri unaozungumzwa hapo, kimsingi neno la kiebrania linalotumika hapo ni “Rûm” ambalo kimatamshi linatamkwa room neno hili lina maana pana zaidi kama nitakavyokuonyesha kwanza tafasiri nyingine za matoleo ya biblia ya kiingereza ili uweze kubaini misamiati tofauti tofauti upate kufaidika na maana halisi ya neno hilo:-

-          King James Version (KJV) – and the Lord hardened the heart of Pharaoh king of Egypt, and he pursued after the children of Israel, and the Children of Israel went out with and high hand

-          English Standard version (ESV) - and the Lord hardened the heart of Pharaoh King of Egypt, and he pursued after the people of Israel while the people of Israel were going out defiantly.

-          The Message Bible (MSG) – God made pharaoh king of Egypt stubborn, determined to chase the Israelites as they walked out on him even without looking Back.

-          God’s word translation (GW) – the Lord made pharaoh (the king of Egypt) stubborn that he pursued the Israelites, who were boldly leaving Egypt.

-          Holman Christian Standard Bible (CSB) – The Lord hardened the heart of Pharaoh king of Egypt and he pursued the Israelites, who were going triumphantly.   

Sikutaka kutumia matoleo mengine ambayo kimsingi yanaweza kuwa yamerudia neno mojawapo kama haya yaliyotumika hapo juu, hivyo nimechagua matoleo ambayo yametumia misamiati mbali mbali tofauti ili tuweze kujifunza kwa upana

1.       High – hand – Mkono ulionyooshwa, kwa nguvu kwa mamlaka, bila kujali hisia zao

2.       Defiantly. – Kwa lazima, kwa kuasi, bila kumtii au kumsikiliza Farao tena

3.       even without looking Back – Bila kutazama nyuma, moja kwa moja bila kujali wala kuhuzunikak

4.       boldly leaving – Kwa ujasiri, Bila kuogopa, bila hofu, ukijua uendako,

5.       triumphantly – Kwa shangwe, kwa furaha, kwa ushindi wa kufikia malengo

Rûm – Kwa ujeuri sasa maana yake kwa mkono wa Bwana ulionyooshwa, Kwa nguvu na mamlaka ya Mungu, wakati wao wanaomboleza kwa misiba, Israel anasonga mbele, Kwa lazima, kwa kuasi amri ya Farao, bila matakwa yake, bila kumsikiliza, bila kumtii, kwa kuinuliwa juu kulikopitiliza, bila kutazama nyuma, wala mpango wa kurejea tena, moja kwa moja bila kujali ya nyuma, kwa ujasiri, bila woga wowote, wakiwa wanajua kule wanakokwenda, sio kwa kubahatisha, kwa furaha na shangwe kwa mikogo, wakiwa na ushindi wa kufikia malengo, wakijivunia walioinuliwa sana, kwa uchangamfu sio kwa machozi. Kwa hiyo wana wa Israel kwao ilikuwa ni siku ya furaha kubwa sana kila mmoja ilikuwa ni shauku yake kuwa ni lini Bwana atakuja kuwatoa watoke katika hali waliyokuwa wakiipitia, walikuwa wamechoshwa na walikuwa sasa imani zao zimepanda sana, Israel walitoka si kwa jeuri yao bali walikuwa wamejaa matumaini, wametiwa nguvu, hawana hofu ya kurejea nyuma, Imani yao ilikuwa imepanda sana saababu kubwa ikiwa ni Mungu wao na namna alivyojifunua kwao kwa mkono wake uliohodari, mkono wa Bwana ulioonyooshwa, Bila hofu kwa ujasiri na kwa kujiamini.

Waebrania 11:27-29 “Kwa imani akatoka Misri, asiogope ghadhabu ya mfalme; maana alistahimili kama amwonaye yeye asiyeonekana. Kwa imani akaifanya Pasaka, na kule kunyunyiza damu, ili yule mwenye kuwaangamiza wazaliwa wa kwanza asiwaguse wao.Kwa imani wakapita kati ya Bahari ya Shamu, kama katika nchi kavu; Wamisri walipojaribu kufanya vivyo wakatoswa.”

Nani ni sababu ya Jeuri yetu.

Israel walitoka kwa nguvu, kwa mamlaka na uthabiti mwingi kama tulivyojifunza hapo juu, sababu kubwa ya ujeuri huu haikuwa jeuri ya kibinadamu bali walikuwa wamejifunza jinsi Mungu alivyo mwema katika njia zake, kadiri alivyojifunua kwao kwa mapigo yale yote kumi, kila pigo lilikuwa ni shuhuda ya kuwa wanaye mtetezi ambaye hakuna anayeweza kupambana naye, ujeuri huu ulikuwa unatokana na nguvu alizonazo Mungu, Mungu wetu miujiza waliyokuwa wameiona ilikuwa imewapa imani thabiti kuwa wanaye Mkombozi, na hivyo hawakua na mashaka naye.

Wamisri pamoja na mfalme wao jeuri waliwasisitiza Israel kundoka maana hali yao ilikuwa mbaya na hawakujua kama watasalimika waliona kuwa wameisha wote hivyo waliwataka waondoke haraka

Kutoka 12:29-33 “Hata ikawa, usiku wa manane BWANA akawapiga wazaliwa wa kwanza wote katika nchi ya Misri, tangu mzaliwa wa kwanza wa Farao aliyeketi katika kiti chake cha enzi, hata mzaliwa wa kwanza wa mtu aliyefungwa katika nyumba ya wafungwa; na wazaliwa wa kwanza wote wa wanyama. Farao akaondoka usiku, yeye na watumishi wake wote, na Wamisri wote; pakawa na kilio kikuu katika Misri; maana hapakuwa na nyumba hata moja asimokufa mtu. Akawaita Musa na Haruni usiku, akasema, Ondokeni tokeni katika watu wangu, ninyi na wana wa Israeli; enendeni, kamtumikieni BWANA kama mlivyosema.Twaeni kondoo zenu na ng'ombe zenu kama mlivyosema, enendeni zenu, mkanibariki mimi pia.Wamisri nao wakawahimiza watu, kuwatoa katika nchi kwa haraka, maana walisema, Tumekwisha kufa sote.”

Mungu alikuwa pamoja nao na wala hakuwaacha wakati wa mchana wala wakati wa usiku, hii iliwapa ujasiri mkubwa sana, Mungu aliwashughulikia vikali maadui wa Israel na alionekana wazi kwa nguzo ya wingu wakati wa mchana na alionekana wazi kwa nguzo ya moto wakati wa usiku na ni yeye mwenyewe ndiye aliyekuwa akiwaongoza njia, Jambo hili liliwapa ujasiri mkubwa sana.

Kutoka 13:21-22. “BWANA naye akawatangulia mchana ndani ya wingu mfano wa nguzo, ili awaongoze njia; na usiku, ndani ya moto mfano wa nguzo, ili kuwapa nuru; wapate kusafiri mchana na usiku; ile nguzo ya wingu haikuondoka mchana, wala ile nguzo ya moto haikuondoka usiku, mbele ya hao watu.”

Hakuna jambo linatupa kiburi kama kujua ya kuwa Bwana yuko pamoja nasi, hakuna jambo linatupa ujasiri kama kujua Neno la Mungu linasema nini juu yetu, hakuna kitu kinatupa kujiamini kama kujua kuwa BWANA ni siri ya wokovu wetu, nuru yetu na ngao yetu, na ulinzi wetu, BWANA ni kila kitu kwetu hakuna jambo linatupa nguvu na mamlaka kama kujua ya kuwa Bwana anatupenda sana, na kuwa yuko upande wetu, hakuna jambo linatupa matumaini kama kujua ya kuwa Mungu ni mtetezi wetu na ya kuwa yuko hai, na yuko pamoja nasi kututetea na kutulinda na kutufunika !

Zaburi 27:1-3 “Bwana ni nuru yangu na wokovu wangu, Nimwogope nani? Bwana ni ngome ya uzima wangu, Nimhofu nani? Watenda mabaya waliponikaribia, Wanile nyama yangu, Watesi wangu na adui zangu, Walijikwaa wakaanguka. Jeshi lijapojipanga kupigana nami, Moyo wangu hautaogopa. Vita vijaponitokea, Hata hapo nitatumaini.”

Ayubu 19:25-27 “Lakini mimi najua ya kuwa Mteteaji wangu yu hai, Na ya kuwa hatimaye atasimama juu ya nchi. Na baada ya ngozi yangu kuharibiwa hivi, Lakini, pasipokuwa na mwili wangu nitamwona Mungu; Nami nitamwona mimi nafsi yangu, Na macho yangu yatamtazama, wala si mwingine. Mtima wangu unazimia ndani yangu.”

Warumi 8:33-39 “Ni nani atakayewashitaki wateule wa Mungu? Mungu ndiye mwenye kuwahesabia haki. Ni nani atakayewahukumia adhabu? Kristo Yesu ndiye aliyekufa; naam, na zaidi ya hayo, amefufuka katika wafu, naye yuko mkono wa kuume wa Mungu; tena ndiye anayetuombea. Ni nani atakayetutenga na upendo wa Kristo? Je! Ni dhiki au shida, au adha, au njaa, au uchi, au hatari, au upanga? Kama ilivyoandikwa, ya kwamba, Kwa ajili yako tunauawa mchana kutwa, Tumehesabiwa kuwa kama kondoo wa kuchinjwa. Lakini katika mambo hayo yote tunashinda, na zaidi ya kushinda, kwa yeye aliyetupenda. Kwa maana nimekwisha kujua hakika ya kwamba, wala mauti, wala uzima, wala malaika, wala wenye mamlaka, wala yaliyopo, wala yatakayokuwapo, wala wenye uwezo, wala yaliyo juu, wala yaliyo chini, wala kiumbe kinginecho chote hakitaweza kututenga na upendo wa Mungu ulio katika Kristo Yesu Bwana wetu.”

Israel walipata Jeuri kwa sababu walijua kuwa Mungu ni Mungu anayesimamia neno lake, na agano lake akitamka kitu ni sheria, lazima kiwe, Mungu wetu ni mwaminifu na hatatuacha, wala hatatuangusha, andiko linasema na kila amwaminiye hatatahayari kamwe. Kama ni hivyo kwanini shetani asituone tuna jeuri, kwanini wapinzani wako wasikuone una jeuri? Kwanini wqasikuone una mikogo kwa sababu Bwana ndiye sababu yetu

Kutoka Misri kwa ujeuri

Neno la Mungu linatukumbusha ya kuwa Mungu ni mwaminifu katika kazi yake ya ukombozi, na kuwa yeye yuko tayari kumtoa kila mmoja katika hali yake ya utumwa, na kutupa ujasiri wa kusonga mbele, wala tusiwe na mashaka naye, kila changamoto unayokutana nayo na inayokutumikisha inataka kukuweka utumwani, na haitaki kukuachia kwa haraka kwa sababu inataka uwe mtumwa wa hali hiyo jambo kubwa la Msingi ni kukumbuka kuwa leo ni siku yako ya kutoka Misri kwa ujeuri, una shuhuda nyingi za jinsi Bwana alivyoyapigania maisha yako na  ya wengine kwa hiyo hauna sababu ya kuogopa au kulia na kuomboleza hata adui akijaribu kukufuata tena anachokitafuta kitampata, Farao alipojaribu kuwafuatia Israel kwa sababu walitoka kwa jeuri maandiko yanasema alifutiliwa mbali yeye na majeshi yake yote, katika biblia ya kiingereza inaonekana vizuri zaidi kuwa Farao pia alifutiliwa mbali kabisa na majeshi yake yote na hakubakia hai ona   

Zaburi 136:13-15 “Yeye aliyeigawa Bahari ya Shamu; Kwa maana fadhili zake ni za milele. Akawavusha Israeli katikati yake; Kwa maana fadhili zake ni za milele. Akamwangusha Farao na jeshi lake katika Bahari ya Shamu; Kwa maana fadhili zake ni za milele.”

Psalm 136:13-15 “to him who divided the Red Sea asunder His love endures forever. And brought Israel through the midst of it, His love endure forever, BUT SWEPT Pharaoh and his army into the Red Sea; His love endure forever

Maandiko yanaonyesha wazi kuwa Majeshi ya wamisri yalifutwa yote sawasawa na neno la Musa mtumishi wa Mungu hapo aliposema hawa mnaowaona leo hamtawaona tena milele, Mwandishi maarufu wa Historia ya wayahudi aitwaye Flavius Josephus alisema kuhusiana na tukio hili nanukuu “And thus did all these men perish, so that there was not one man left to be a messenger of this calamity to the rest of the Egyptians” kwa tafasiri yangu “Na wote wakaangamia hata kusiwepo hata mjumbe wa kuelezea yaliyowakuta wamisri” leo nataka utoke kwa ujasiri katika kila kifungo kinachokuonea, leo nataka kifungo kinachokuonea na kukandamiza kiwe mwisho, na usikione tena leo nataka utoke katika Misri inchi yako ya utumwa kwa ujeuri, utoke nje ya uonevu wa mashetani, nje ya magonjwa, nje ya huzuni, nje ya kila kinachopoteza tumaini la maisha yako, Nje ya utasa wako, nje ya kansa, nje ya tezi dume, nje ya magonjwa ya kizee, nje ya umasikini, nje ya uonevu wa wachawi, nje ya vifungo vya nguvu za giza, nje ya mashambulizi na uonevu wa ibilisi, leo nakutangazia kwa mamlaka niliyopepewa kama mtumishi wake kwa mafuta aliyonipaka kwayo nasema  Toka kwa imani ukimtegema Mungu na kufahamu ya kuwa hatakuangusha, mtegemee yeye katika maamuzi makubwa ya maisha, uwe na ujasiri unapopita katika dhiki na shida, kabiliana na majaribu yako kwa Imani ukijua wazi hatimaye Mwokozi atasimama karibu nawe na kukutoa katika hali unayoipitia na kamwe usitazame nyuma, toka kwa ujeuri mbele kwa mbele usitazame tena jaribu lako na nakuhakikishia halitakuwepo tena!, Bwana ameniambia kuwa fadhili zake ni za milele, ikiwa aliwaokoa wana wa Israel wakatoka kwa Jeuri, leo ni zamu yako kutoka kwa ujeuri katika hali iliyokusumbua kwa miaka mingi, katika jina la Yesu Kristo pokea, mahitaji yako, pokea uzima wako, pokea ukombozi wako, pokea uhai wako, nakufungua na kukuweka mbali na mauti katika jina la Yesu Kristo nakutamkia uzima kwa mamlaka niliyo nayo katika jina la Yesu, pepo achia wasomaji wangu, achilia wasikilizaji wangu, achilia watu wa Mungu katika jina la Yesu, Nakutangazia kutoka kwa Jeuri na kumuacha Shetani akijuta na kusikitika kwa kukuachia na akijaribu kukufuata ataangamia kama Farao katika jina la Yesu Kristo Mwana wa Mungu aliye hai! Ramashakatariboso, saparatashanda, rimosakata free sakata lota fakaseta rimoso pa taratshatata parafata, katika jina la Yesu Amen!

 

Rev. Innocent Samuel Kamote.

Mkuu wa wajenzi mwenye Hekima.

Hakuna maoni: