Alhamisi, 13 Machi 2025

Umuhimu wa kuwa na Amani na watu wote!


Waebrania 12:14-15 “Tafuteni kwa bidii kuwa na amani na watu wote, na huo utakatifu, ambao hapana mtu atakayemwona Bwana asipokuwa nao; mkiangalia sana mtu asiipungukie neema ya Mungu; shina la uchungu lisije likachipuka na kuwasumbua, na watu wengi wakatiwa unajisi kwa hilo.”




Utangulizi:

Moja ya kanuni za muhimu sana katika ufalme wa Mungu ni pamoja na swala zima la kuhakikisha kuwa unakuwa na amani na watu wote, Maandiko yanatoa wito wa kufanya bidii kutafuta Amani na watu wote, Hili ni jambo la Msingi, Kwa kuwa tuko duniani kuzuka na kutokea kwa migogoro ni swala la kawaida sana katika jamii hususani watu wanapoishi pamoja, lakini hata hivyo kama watu wa Mungu au watu wenye ukomavu hatupaswi kuiacha migogoro hiyo ikadumu kwa Muda mrefu na kuwatia unajisi watu wengine, Migogoro katika maandiko inafananishwa na shina la uchungu, shina ni chanzo, na kwa sababu hiyo mti wowote ambao shina lake litakuwa chungu, ni rahisi mti huo kueneza uchungu katika matawi yake na au hata katika matunda yake na kwa sababu hiyo katika ukuaji wa kiroho migogoro huathiri utiririkaji wa neema ya Mungu na kuleta upungufu wa neema ya Mungu katika maisha ya waamini, Lakini tunapofanya bidii ya kutafuta Amani tunazuia uchungu huo na kujiimarisha kuwa wana wa Mungu

Mathayo 5:9 “Heri wapatanishi; Maana hao wataitwa wana wa Mungu.” Neno wapatanishi hapo katika lugha ya asili ya kiyunani linasomeka kama “eirēnopoios” kwa kiingereza “peacemakers” wanaosababisha amani itokee au iwepo hao ni watu wenye baraka kubwa, wamebarikiwa sana kama maandiko yanenavyo na kiyume chake wanaosababisha makwazo wanaitwa ole yaani waliolaaniwa na ambao adhabu kubwa sana inaweza kuwakabili.

Luka 17:1-4 “Akawaambia wanafunzi wake, Makwazo hayana budi kuja, lakini ole wake mtu yule ambaye yaja kwa sababu yake! Ingemfaa zaidi mtu huyo jiwe la kusagia lifungwe shingoni mwake, akatupwe baharini, kuliko kumkosesha mmojawapo wa wadogo hawa. Jilindeni; kama ndugu yako akikosa, mwonye; akitubu msamehe. Na kama akikukosa mara saba katika siku moja, na kurudi kwako mara saba, akisema, Nimetubu, msamehe.”

Wakiyajua haya wazee wetu wa imani zamani sio kuwa hawakuwahi kukutana na migogoro ya ina mbalimbali walikutana nayo lakini walikuwa na bidii kuhakikisha kuwa wanarejesha amani au kuepusha kabisa migogoro miongoni mwao wakitumia busara kubwa sana, kwa sababu hiyo maandiko yanamtaka kila mmoja wetu kuhakikisha kuwa anatunza amani kila wakati kunapotokea migogoro ya aina mbalimbali au kuzima kwa haraka migogoro na vyanzo vinavyoashiria kutoweka kwa Amani kabla mambo hayajaharibika kabisa, Katika maandiko iko mifano ya watu kama kina Abrahamu, Isaka, na Yakobo na wengineo ambao kwa namna moja ama nyingine walifanya kila jitihada ya kuhakikisha kuwa wanadhibiti migogoro na kutafuta Amani ya kudumu katika maisha yao ya uchaji Mungu na uhusiano na watu wengine, tutajifunza somo hili umuhimu wa kuwa na amani na watu wote kwa kuzingatia vipengele vitatu vifuatavyo:-

·         Mifano ya wazee waliotafuta kuwa na amani na watu wote

·         Baraka ya kuwa na amani na watu wote

·         Umuhimu wa kuwa na amani na watu wote  


Mifano ya wazee waliotafuta kuwa na amani na watu wote.

Neno Amani linalotumika katika maandiko kwa agano la kale linatumika neno la kiibrania “Shālōm” na katika maandiko ya agano jipya linatumika neno “eirēne” kimatamshi “Irene” maneno haya katika tafasiri ya kiingereza maana yake ni “it is a condition of being freedom from any kind of disturbance wether outwardly or inwardly” yaani ni hali ya kuwa mbali na usumbufu wa aina yoyote wa nje au wa ndani, usumbufu huu unaweza kuwa wa nafsi au familia, au taifa na kadhalika, neno hilo Shālōm pia lilitumiwa na Wayahudi kumtakia mtu mafanikio ya kimwili na kiroho na lilitumika katika matumizi ya kila siku ya kumtakia mtu mema wakati wa salamu, kwa hiyo hii hasa ndio Amani na utulivu au hali ya kutokuwa na vita au uhasama au ugomvi na mtu na hii ndio Amani ambayo maandiko yanaagiza tuwe nayo na watu wote, Amani hii ni msingi mkubwa wa mafanikio na ustawi mkubwa wa mwanadamu popote alipo duniani.

Maandiko yana mifano mingi inayoonyesha kuwa wazee wetu katika kusafiri kwao duniani walikutana na changamoto za namna mbalimbali ambazo zingeweza kuharibu amani na maisha yao pia, lakini katika namna ya kushangaza sana maandiko yanatuonyesha namna na jinsi wazee wetu walivyokuwa na busara na hekima iliyopelekea wao kuepusha changamoto za aina mbalimbali ambazo zingeweza kuwa sababu ya ukosefu wa amani katika maisha yao duniani na kwa sababu hiyo walifanya kila linalowezekana kuhakikisha kuwa wanapata Amani hata pale ilipotokea wamehitilafiana na mtu, hapa iko mifano kadhaa ya watu walioitafuta Amani kwa bidi ona:-

Mfano wa Ibrahimu na Lutu.

Mwanzo 13:5-12 “Na Lutu aliyesafiri pamoja na Abramu, yeye naye alikuwa na makundi ya ng'ombe na kondoo, na hema. Na ile nchi haikuwatosha, ili wakae pamoja; maana mali zao zilikuwa nyingi, hata wasiweze kukaa pamoja. Kukawako ugomvi kati ya wachunga wanyama wa Abramu, na wachunga wanyama wa Lutu; na siku zile Wakanaani na Waperizi walikuwa wakikaa katika nchi. Abramu akamwambia Lutu, Basi, usiwepo ugomvi, nakusihi, kati ya mimi na wewe, wala kati ya wachungaji wangu na wachungaji wako; maana sisi tu ndugu. Je! Nchi hii yote haiko mbele yako? Basi ujitenge nami, nakusihi; ukienda upande wa kushoto, nitakwenda upande wa kuume; ukienda upande wa kuume, nitakwenda upande wa kushoto. Lutu akainua macho yake, akaliona Bonde lote la Yordani, ya kwamba lote pia lina maji, kabla BWANA hajaharibu Sodoma na Gomora, lilikuwa kama bustani ya BWANA, kama nchi ya Misri hapo unapokwenda Soari. Basi Lutu akajichagulia Bonde lote la Yordani; Lutu akasafiri kwenda upande wa mashariki; wakatengana wao kwa wao. Abramu akakaa katika nchi ya Kanaani, na Lutu akakaa katika miji ya lile Bonde; akajongeza hema yake mpaka Sodoma.”

Wachungaji wa Abrahamu na Lutu walianza kugombana kwa sababu mifugo yao ilikuwa imeongezeka sana kiasi ambacho nchi ilikuwa haiwatoshi kwa sababu walikaa pamoja, Abrahamu aliona wazi kuwa jambo hili lisingelileta matokeo mema na kwa sababu hiyo alimwita Lutu na kutoa mapendekezo kwa kumsihi ajitenge naye, Abrahamu hakuwa na choyo wala ubinafsi alimpa Lutu chaguo la kwanza kuchagua na kumueleza wazi kuwa endapo atachagua kwenda kushoto yeye atakwenda kulia na akichagua kwenda kulia yeye atachagua kwenda kushoto, hakukuwa na ubinafsi moyoni lakini msingi mkuu ulikuwa ni USIWEPO UGOMVI KATI YA MIMI NA WEWE  MAANA SISI NI NDUGU, Abrahamu aliipa Amani kipaumbele cha kwanza kuliko maslahi binafsi. Aliamini kuwa Mungu atambariki vyovyote iwavyo bila kujali chaguo lake litamuathiri kwa kiwango gani:-

Amani ya kweli haipatikani kwa kushinda siku zote inapatikana kwa unyenyekevu na kuwa tayari kupoteza haki zako na wakati mwingine hata mazuri tuliyokuwa tukiyatarajia kwa faida ya Amani yenyewe kuliko mafarakano, Amani wakati mwingine inatutaka kumuachia Mungu na sisi kujitoa ili Amani iwe faida ya pande zote mbili, kumpata ndugu yako ni kwa muhimu sana kuliko faida za ubinafsi na tamaa ya moyo! Nyakati tulizo nazo leo wako watu ambao wako tayari kupoteza ndugu na marafiki kuliko kuitafuta Amani, Maandiko yanatufunza kuwa Amani ni ya muhimu kuliko kupoteza ndugu au rafiki na hiki ndio Abrahamu anatufundisha katika maisha yake.

1Wakorintho 8:13 “Kwa hiyo, chakula kikimkwaza ndugu yangu, hakika sitakula nyama hata milele, nisije nikamkwaza ndugu yangu.”

Mfano wa Isaka na Wafilisti (wenyeji).

Mwanzo 26:12-22 “Isaka akapanda mbegu katika nchi ile, akapata mwaka ule vipimo mia kwa kimoja, BWANA akambariki. Na mtu huyu akawa mkuu, akazidi kusitawi, hata akawa mkuu sana. Akawa na mali ya kondoo, na mali ya ng'ombe, na watumwa wengi. Hao Wafilisti wakamhusudu. Na vile visima vyote walivyochimba watumwa wa baba yake, siku za Ibrahimu babaye, Wafilisti walikuwa wamevifukia, wakavijaza kifusi. Abimeleki akamwambia Isaka, Utoke kwetu, maana wewe una nguvu sana kuliko sisi. Basi Isaka akatoka huko akapiga kambi katika bonde la Gerari, akakaa huko. Isaka akarudi akavichimbua vile visima vya maji walivyovichimba siku za Ibrahimu babaye; maana wale Wafilisti walikuwa wamevifukia baada ya kufa kwake Ibrahimu; naye akaviita majina kufuata majina alivyoviita babaye. Watumwa wa Isaka wakachimba katika lile bonde, wakapata kisima cha maji yanayobubujika. Wachungaji wa Gerari wakagombana na wachungaji wa Isaka wakisema, Maji haya ni yetu. Ndipo akakiita jina la kile kisima Eseki, kwa sababu waligombana naye. Wakachimba kisima kingine, wakagombania na hicho tena. Akakiita jina lake Sitna. Akaondoka huko akachimba kisima kingine, wala hicho hawakukigombania. Akakiita jina lake Rehobothi, akasema, Kwa kuwa sasa BWANA ametufanyia nafasi, nasi tutazidi katika nchi.”

Isaka alikuwa na mafanikio makubwa sana alistawi mno, jambo hili liliamsha wivu kwa wenyeji yaani wafilisti walijaribu kutafuta na kufukia siri ya mafanikio ya Isaka, Isaka alikuwa akichimba visima yeye na Abrahamu baba yake walikuwa na ujuzi wa kuchimba visima, Isaka alipata visima vilivyobubujisha maji na hivyo alivitumia kwa umwagiliaji na unyweshaji wa mifugo na kwa sababu hiyo alifanikiwa na kustawi sana, wenyeji waliona wivu, waliogopa mafanikio yake walimuogopa na yeye pia lakini pia walimsumbua walianza kufukia visima hivyo kwa uchafu wakimlazimisha kuchimba vingine, hata hivyo kila alipochimba kisima kingine Wafilisti walikigombania na kudai kuwa kisima ni chao!

Isaka hakupambana nao wala hakutaka kulipa kisasi wala kutafuta ushahidi kuwa visima vilikuwa mali ya baba yake na badala yake alihama na kuchimba kisima kingine alifanya hivyo kila mara walipofukia kisima chake au kukigombania kwa kudai kuwa ni mali yao, hatimaye alichimba kingine tena na kingine tena na kingine tena na hatimaye mwisho wakaona aibu wala hawakukigombania tena akakiita kisima hicho “Rehoboth” maana yake Bwana ametufanyia nafasi, na wafilisti hawakukigombania tena.

Isaka aliipata Amani yake kwa kukubali kuachilia na kupoteza, alijitahidi kila wakati kuepuka migogoro isiyo na sababu za kimsingi ambayo yeye aliona itavuruga Amani na hivyo aliamua kutumia nafasi ya kuachilia (withdraw) au kujiepusha, wakati mwingine ili kuipata Amani itatugharimu kuachilia, itatugharimu kwenda mbali ili kuepusha migogoro badala ya kusisitiza haki zetu, hatimaye Mungu ataongeza neema kwa wale wanaotafuta amani kwa bidii na kwa mioyo yao

1Petro 3:10-12 “Kwa maana, Atakaye kupenda maisha, Na kuona siku njema, Auzuie ulimi wake usinene mabaya, Na midomo yake isiseme hila. Na aache mabaya, atende mema; ATAFUTE AMANI, AIFUATE SANA. Kwa kuwa macho ya Bwana huwaelekea wenye haki, Na masikio yake husikiliza maombi yao; Bali uso wa Bwana ni juu ya watenda mabaya.”

Mfano wa Yakobo na Labani

Mwanzo 31:22-55 “Hata siku ya tatu Labani akaambiwa ya kwamba Yakobo amekimbia, akatwaa ndugu zake pamoja naye, akamfuata mwendo wa siku saba. Akampata katika mlima wa Gileadi. Mungu akamjia Labani, Mshami, katika ndoto ya usiku, akamwambia, Ujihadhari, usimwambie Yakobo neno la heri wala la shari. Labani akamfikia Yakobo, na Yakobo alikuwa amepiga hema zake katika mlima, na Labani na ndugu zake wakapiga hema zao katika mlima wa Gileadi. Labani akamwambia Yakobo, Umefanya nini? Umenihadaa, ukawachukua binti zangu kama mateka waliotwaliwa kwa upanga. Mbona umekimbia kwa siri ukanihadaa, wala hukuniambia, nipate kuagana nawe uende zako kwa furaha, na nyimbo, na ngoma, na kinubi? Wala hukuniacha niwabusu wanangu, na binti zangu; basi umetenda upumbavu. Ninao uwezo mkononi mwangu wa kukufanyia madhara; lakini Mungu wa baba yako usiku huu ameniambia, akisema, Ujihadhari, usimwambie Yakobo neno la heri wala la shari. Basi sasa, umetoka kwa sababu umetamani sana nyumba ya baba yako. Mbona basi umeiiba miungu yangu? Yakobo akajibu, akamwambia Labani, Kwa sababu naliogopa, nikasema, Usije ukaninyang'anya binti zako kwa nguvu. Awaye yote utakayemwona kuwa nayo miungu yako, yeye asiishi. Mbele ya ndugu zetu ukitambue kilicho chako kwangu, ukakichukue. Maana Yakobo hakujua ya kwamba Raheli ameiiba. Labani akaingia katika hema ya Yakobo, na hema ya Lea, na hema ya vijakazi wawili, wala hakuiona. Akatoka katika hema ya Lea, akaingia katika hema ya Raheli. Basi Raheli alikuwa amevitwaa vile vinyago ameviweka katika matandiko ya ngamia, na kuvikalia. Labani akapapasa hema yote wala hakuviona. Naye Raheli akamwambia babaye, Bwana wangu asikasirike kwa sababu siwezi kuinuka mbele yako, maana nimeshikwa na mambo ya kike. Akatafuta, wala hakuviona vile vinyago. Yakobo akakasirika, akagombana na Labani. Yakobo akajibu, akamwambia Labani, N'nini hatia yangu? Nayo ni nini dhambi yangu, hata ukanifuatia namna hii? Umepapasa-papasa vyombo vyangu vyote; ni kitu gani ulichokiona cha nyumbani mwako? Kiweke hapa mbele ya ndugu zangu, na ndugu zako, wakaamue kati yetu. Miaka hii ishirini nimekaa kwako; kondoo zako wala mbuzi zako wake hawakuharibu mimba wala waume katika wanyama wako sikuwala. Kilichoraruliwa na hayawani sikukuletea, mimi mwenyewe nimetwaa hasara yake, wewe umekidai katika mkono wangu, ikiwa kilichukuliwa mchana, au ikiwa kilichukuliwa usiku. Hii ilikuwa hali yangu; mchana jua likanipata, na baridi usiku, usingizi ukanitoka machoni mwangu. Miaka hii ishirini nimekaa nyumbani mwako; nilikutumikia miaka kumi na minne kwa binti zako wawili, na miaka sita kwa wanyama wako, nawe umebadili mshahara wangu mara kumi. Kama Mungu wa baba yangu, Mungu wa Ibrahimu na Hofu ya Isaka, hangalikuwa pamoja nami, hakika sasa ungalinifukuza mikono mitupu. Mateso yangu na kazi za mikono yangu Mungu ameziona, akakukemea usiku huu. Labani akajibu, akamwambia Yakobo, Hao binti ni binti zangu, na wana ni wanangu, na wanyama ni wanyama wangu, na yote uyaonayo ni yangu; nami naweza kuwatendea nini leo binti zangu na wana wao waliowalea? Haya! Na tufanye agano, mimi na wewe, liwe kwa ushahidi kati ya mimi na wewe. Yakobo akatwaa jiwe akalisimamisha kama nguzo. Yakobo akawaambia ndugu zake, Kusanyeni mawe. Wakatwaa mawe, wakafanya chungu, nao wakala huko karibu na ile chungu. Labani aliiita Yegarsahadutha, lakini Yakobo aliiita Galedi. Labani akasema, Chungu hii ni shahidi kati ya mimi na wewe hivi leo. Kwa hiyo likaitwa jina lake Galedi, na Mispa, maana alisema, Mungu avizie kati ya mimi na wewe, wakati tusipoonana. Ukiwatesa binti zangu, na ukitwaa wake zaidi ya binti zangu, wala hapana mtu pamoja nasi, tazama, Mungu ni shahidi kati ya mimi na wewe. Labani akamwambia Yakobo, Tazama chungu hii utazame na nguzo niliyoitia kati ya mimi na wewe.  Chungu hii na iwe shahidi, na nguzo hii na iwe shahidi, ya kuwa mimi sitapita chungu hii kuja kwako, wala wewe hutapita chungu hii na nguzo hii uje kwangu, kwa madhara. Mungu wa Ibrahimu, na Mungu wa Nahori, Mungu wa baba yao, ahukumu kati yetu. Yakobo akachinja sadaka katika mlima, akawaita ndugu zake waje wale chakula, nao wakala chakula, wakakaa usiku kucha mlimani. Labani akaondoka asubuhi na mapema, akawabusu wanawe na binti zake, akawabariki; kisha Labani akaenda zake, akarudi kwao.”

Mgogoro wa Yakobo na Labani ulikuwa mgogoro mkubwa sana Mtu ameishi kwa mjomba wake mwenye hila nyingi ambaye amemfanyia uonevu wa kila aina, Maandiko yanaweka wazi kuwa Labani alijaribu kumrubuni Yakobo mara nyingi sana huku akibadilisha mshahara wake zaidi ya mara kumi, Hali ya maisha katika nyumba ya Labani ilikuwa ngumu mno kiasi ambacho Yakobo aliamua kutoroka unaweza kuona na kuwaza mtu anamtoroka mjomba wake kwa siri, huku hakukuwa kuachana kuzuri kwa watu ambao ni ndugu hata hivyo Labani alibaini na kumfuatia Yakobo akiwa amejawa na hasira nyingi, bila kujali kuwa amemrubuni Yakobo na kuyatumia maisha ya ujana wake wote kwa faida zake.

Baada ya kukabiliana kwa maneno makali hatimaye Yakobo na Labani waliamua kufanya agano ili kwamba asiwepo mtu atakayempandia mwenzake kwa madhara, Waliamua kusimamisha jiwe kubwa kama Ushahidi na kulitia mafuta kwamba hakuna mtu aatakayelivuka jiwe hilo kumuendea mwenzake kwa madhara, Jiwe hilo liliwahakikishia Amani na usalama licha ya kuwa walikuwa wamejeruhiana moyo kwa siku nyingi na kwa maumivu makubwa, lakini waliamua kuiacha Amani ishinde na kila mmoja kuendelea na maisha yake.

Wakati mwingine ili Amani ipatikane hatuna budi kukabiliana na mtu uso kwa uso, na kuyazungumza na kupata suluhu na makubaliano, Amani inahitaji watu wasameheane, na kujiwekea mipaka ili Amani iweze kuwepo, Haikuwa rahisi kuipata Amani ukiwa na mjomba kama Labani, Lakini Labani licha ya kuonywa na Mungu alikumbuka kuwa Yakobo pia ni mkwewe na mali alizonazo pia ni za wanae na wajukuu zake, waliamua kumaliza tofauti zao.

Mfano wa Yakobo na Esau.

Mwanzo 32:6-11 “Wale wajumbe wakarudi kwa Yakobo wakisema, Tulifika kwa ndugu yako, Esau, naye anakuja kukulaki, na watu mia nne pamoja naye. Ndipo Yakobo akaogopa sana, na kufadhaika sana, akawagawanya watu waliopo pamoja naye, na kondoo, na ng'ombe, na ngamia, wawe matuo mawili. Akasema, Akija Esau kwa kundi la kwanza, akalipiga, kundi litakalosalia litaokoka. Yakobo akasema, Ee Mungu wa baba yangu Ibrahimu, na Mungu wa baba yangu Isaka, BWANA, uliyeniambia, Rudi uende mpaka nchi yako, na kwa jamaa zako, nami nitakutendea mema; mimi sistahili hata kidogo hizo rehema zote na kweli yote uliyomfanyia mtumwa wako; maana nalivuka mto huo wa Yordani na fimbo yangu tu, na sasa nimekuwa matuo mawili. Uniokoe sasa na mkono wa ndugu yangu, mkono wa Esau, maana mimi namwogopa, asije akanipiga, na mama pamoja na wana. Walikuwa ni watu ndugu mapacha waliokuja kuumizana sana, Yakobo alinunua kwa hila haki ya mzaliwa kwa kwanza ya Esau, kama haikutosha Yakobo aliiba mbaraka wa mzaliwa wa kwanza waliachana kwa uchungu mkubwa sana Esau akiapa kuwa atamuua Yakobo, baada ya miaka mingi sana Yakobo alipokuwa akirejea alihofia kwamba Esau atalipa kisasi

Yakobo na Esau waliachana vibaya sana, ni mapacha ni ndugu wote wameokoka lakini Yakobo kwa hila alinunua haki ya mzaliwa wa kwanza na baadaye kuchukua mbaraka wa mzaliwa wa kwanza, jambo ambalo lilimuudhi sana Esau ambaye aliapa kuwa angemuua Yakobo, wakati Yakobo anarejea nyumbani alipatwa na hofu kuwa huenda ndugu yake anakuja kumuua, matukio mabaya na kuachana vibaya kuliweka jeraha kubwa sana katika maisha yao Yakobo alimuomba Mungu kwaajili ya hofu hiyo.

Yakobo alitumia zawadi, alitumia maombi kwa Mungu, na aliamua kujinyenyekeza sana na kuinama mbele ya Esau mara saba  kwa hiyo badala ya Esau kumshambulia alimkimbilia na kumkumbatia na kisha wote wakapaza sauti na kulia, bila kujali yaliyojiri, walihitimisha mkasa wao kwa kupatana, walichagua Amani badala ya visasi na viapo vya kumalizana

Amani ya kweli ili ipatikane inahitaji kujinyenyekeza, toba na kumuomba Mungu, sio hivyo tu na kuwa na bidii ya kuitafuta, kumuomba Mungu ni kwa Muhimu kwa sababu Mungu anaweza kuponya majeraha ya ndani kabisa na kujenga tena uhusiano mpya na kuponya majeraha yote ya ndani tunapochukua hatua ya kuitafuta Amani. Fikiria namna Yakobo alivyotanguliza zawadi nyingi na jinsi alivyojinyenyekesha sana na Fikiria Esau alivyoahirisha mpango wake wa kumuua Yakobo, wakati mwingine ni lazima kujishusha, kununua moyo na nduguyo kwa zawadi na kuonyesha heshima kubwa sana gharama hizo ndio bidii inayotajwa katika maandiko ya kwamba sio kila wakati kuitafuta Amani linaweza kuwa jambo rahisi. Lakini inatulazimu kuitafuta Amani kama agizo la Mungu lilivyo.
 

Baraka ya kuwa na amani na watu wote 

Kuwa na Amani na watu wote ni jambo lenye Baraka kubwa sana, linaleta ustawi wa kimwili na kiroho kwa wale wanaotafuta Amani, lakini kisaikolojia na kimwili kuwa na Amani kunapunguza migandamizo ya mawazo, kunakupa Amani ya moyo inayokufanya kuendelea kukua kiroho na kiakili, kujenga uhusiano mwema na watu, kuleta ukomavu na ukuaji wa kiroho, kujenga furaha, kuondoa mashaka, kuleta utulivu na furaha, mawasilano mazuri msamaha, na kujenga mazingira ya Amani na utulivu, ziko faida kadhaa za kibiblia pia ambazo zinatokana na kuweko kwa Amani, kama ifuatavyo:-

1.       Uhusiano wako na Mungu kuimarika - 1Yohana 2:9-11 “Yeye asemaye kwamba yumo nuruni, naye amchukia ndugu yake, yumo gizani hata sasa. Yeye ampendaye ndugu yake, akaa katika nuru, wala ndani yake hamna kikwazo. Bali yeye amchukiaye ndugu yake, yu katika giza, tena anakwenda katika giza, wala hajui aendako, kwa sababu giza imempofusha macho.”

 

2.       Kukubaliwa kwa sadaka zako – Mathayo 5:23-26 “Basi ukileta sadaka yako madhabahuni, na huku ukikumbuka ya kuwa ndugu yako ana neno juu yako, iache sadaka yako mbele ya madhabahu, uende zako, upatane kwanza na ndugu yako, kisha urudi uitoe sadaka yako. Patana na mshitaki wako upesi, wakati uwapo pamoja naye njiani; yule mshitaki asije akakupeleka kwa kadhi, na kadhi akakupeleka kwa askari, ukatupwa gerezani. Amin, nakuambia, Hutoki humo kamwe hata uishe kulipa senti ya mwisho.”

 

3.       Kusikilizwa kwa maombi yako – 1Petro 3:7 “Kadhalika ninyi waume, kaeni na wake zenu kwa akili; na kumpa mke heshima, kama chombo kisicho na nguvu; na kama warithi pamoja wa neema ya uzima, kusudi kuomba kwenu kusizuiliwe.”

 

4.       Kusamahehewe dhambi zako – Marko 11:25-26 “Nanyi, kila msimamapo na kusali, sameheni, mkiwa na neno juu ya mtu; ili na Baba yenu aliye mbinguni awasamehe na ninyi makosa yenu. Lakini kama ninyi hamsamehe, wala Baba yenu aliye mbinguni hatawasamehe ninyi makosa yenu.] ”            

 

5.       Shina la uchungu lisije likasumbua wengi – Shina la uchungu kwa kiyunani ni “Pikria” kwa kiingereza ni “bitterness” au uchungu, kwa kawaida shina au mzizi ndio unaosambaza maji na virutubisho katika mmea na majani sisi kama mwili wa Kristo ni kama mti, shina linapokuwa la uchungu, uchungu huo unasambaa na kuwanajisi wengine, Neno la Mungu linatutaka tuwe na Amani na watu wote ili kuepusha kuwanajisi wengine kwa sababu ya uchungu na ugomvi na ushindani walio nao watu wengine, na kupungukiwa na neema ya Mungu katika maisha yetu.

 

Waebrania 12:14-15 “Tafuteni kwa bidii kuwa na amani na watu wote, na huo utakatifu, ambao hapana mtu atakayemwona Bwana asipokuwa nao; mkiangalia sana mtu asiipungukie neema ya Mungu; shina la uchungu lisije likachipuka na kuwasumbua, na watu wengi wakatiwa unajisi kwa hilo.”

 

6.       Kuonyesha ujuzi wako wa kumjua Mungu - 1Yohana 4:8-12 “Yeye asiyependa, hakumjua Mungu, kwa maana Mungu ni upendo. Katika hili pendo la Mungu lilionekana kwetu, kwamba Mungu amemtuma Mwanawe pekee ulimwenguni, ili tupate uzima kwa yeye. Hili ndilo pendo, si kwamba sisi tulimpenda Mungu, bali kwamba yeye alitupenda sisi, akamtuma Mwanawe kuwa kipatanisho kwa dhambi zetu. Wapenzi ikiwa Mungu alitupenda sisi hivi, imetupasa na sisi kupendana. Hakuna mtu aliyemwona Mungu wakati wo wote. Tukipendana, Mungu hukaa ndani yetu, na pendo lake limekamilika ndani yetu.”   

                 

Umuhimu wa kuwa na amani na watu wote. 

Ni jambo la kusikitisha kuona na kusikia kila mahali siku hizi watu wa Mungu wakiwa mstari wa mbele kwa migogoro, kila mahali siku hizi inaumiza kusikia kuwa mtumishi huyu hapatani na huyu, au askofu huyu ana bifu na huyu, Mchungaji huyu haviivi chungu kimoja na yule, tungetarajia migogoro  na mafarakano kuwa kwa washirika wachanga au kwa watu wasiomjua Mungu, lakini jambo la kusikitisha ni kuwa migogoro mingi leo inaongozwa na watu wa Mungu tena wale ambao ni viongozi, au wako katika nafasi ya wao kuwa wapatanishi, au waamuzi, Inasikitisha kuona leo Mshirika na Mchungaji wake wana ugomvi, inasikitisha kuona mtu ana ugomvi wa miaka na miaka na mtu mwingine na hawamalizi alafu ni watu wa Mungu inaumiza sana sana kuona watu wa Mungu wakiwa hawataki suluhu leo,  Najua kuwa maandiko yanaeleza wazi kuwa siku za mwisho kutakuwa nyakati za hatari na tabia nyingi mbaya zitajitokeza lakini hata hivyo hayo hayapaswi kuwatokea watu wa Mungu kwa sababu maandiko yametujulisha kila kitu kwa uwazi lakini kama watu wa Mungu watakuwa hivyo ni wazi kuwa hakuwezi kuwa na mbingu ya watu wenye mafarakano na nadhani wote wanaweza kuachwa aliyekwazwa na aliyekwaza pia.

2Timotheo 3:1-5 “Lakini ufahamu neno hili, ya kuwa siku za mwisho kutakuwako nyakati za hatari. Maana watu watakuwa wenye kujipenda wenyewe, wenye kupenda fedha, wenye kujisifu, wenye kiburi, wenye kutukana, wasiotii wazazi wao, wasio na shukrani, wasio safi, wasiowapenda wa kwao, wasiotaka kufanya suluhu, wasingiziaji, wasiojizuia, wakali, wasiopenda mema, wasaliti, wakaidi, wenye kujivuna, wapendao anasa kuliko kumpenda Mungu; wenye mfano wa utauwa, lakini wakikana nguvu zake; hao nao ujiepushe nao.”

Haiwezekani watu wa Mungu wanaolijua neno la Mungu na tena wanaolihubiri na kulifundisha kisha wakawa hawataki Amani inasikitisha sana na tujifunze kutoka kwa wazee wetu wa Imani ambao wao walikutana na changamoto mbali mbali lakini walihakikisha kuwa wanakuwa na amani na watu wote, tukumbuke kuwa bila unyenyekevu sio rahisi kuwa na amani, bila kujishusha na kukubali kupoteza haki zako na kuachilia hatuwezi kuwa na Amani, kuipata Amani ni gharama, lakini kama tukiweka ubinasfi na maslahi yetu sio rahisi kuipata Amani, tukikosa uvumilivu na subira ni ngumu kuwa na amani, tukiwa hatuna msamaha na kuikiishi bila mipaka ni vigumu kwetu kuwa na amani, bila kuachilia hatuwezi kuwa na Amani, bila kupoteza hatuwezi kuwa na Amani, haijalishi nani mkubwa nani mdogo bila kuchukua hatua za kipatanishi na maridhiano na urejesho ni vigumu kuwa na amani neno la Mungu limetuagiza kuwa na amani na watu wote hivyo hatuna budi kulitii na kulifanyia kazi tafuta Amani:-

Warumi 12:17-21 “Msimlipe mtu ovu kwa ovu. Angalieni yaliyo mema machoni pa watu wote. Kama yamkini, kwa upande wenu, mkae katika amani na watu wote. Wapenzi, msijilipize kisasi, bali ipisheni ghadhabu ya Mungu; maana imeandikwa, Kisasi ni juu yangu mimi; mimi nitalipa, anena Bwana. Lakini, Adui yako akiwa na njaa, mlishe; akiwa na kiu, mnyweshe; maana ufanyapo hivyo, utampalia makaa ya moto kichwani pake.Usishindwe na ubaya, bali uushinde ubaya kwa wema.”

Amani haiwezi kuja yenyewe ni Lazima itafutwe, na ndio maana Mungu katika hekima yake anatuagiza katika neno lake anawaagiza wenye haki waitafute Amani

Zakaria 8:16-23 “Haya ndiyo mtakayoyatenda; kila mtu na aseme kweli na jirani yake; hukumuni kweli na hukumu ya amani malangoni mwenu; wala mtu wa kwenu asiwaze mabaya moyoni mwake juu ya jirani yake; wala msipende kiapo cha uongo; maana hayo yote ndiyo niyachukiayo, asema Bwana. Tena neno la Bwana wa majeshi likanijia, kusema, Bwana wa majeshi asema hivi, Saumu ya mwezi wa nne, na saumu ya mwezi wa tano, na saumu ya mwezi wa saba, na saumu ya mwezi wa kumi, zitakuwa furaha na shangwe, na sikukuu za kuchangamkia, kwa nyumba ya Yuda; basi zipendeni kweli na amani. Bwana wa majeshi asema hivi, Itatokea halafu ya kwamba watakuja mataifa na wenyeji wa miji mingi; wenyeji wa mji huu watauendea mji huu, wakisema, Haya! Twendeni zetu kwa haraka tuombe fadhili za Bwana, na kumtafuta Bwana wa majeshi; Mimi nami nitakwenda. Naam, watu wa kabila nyingi na mataifa hodari watakuja Yerusalemu kumtafuta Bwana wa majeshi, na kuomba fadhili za Bwana. Bwana wa majeshi asema hivi, Siku hizo watu kumi, wa lugha zote za mataifa, wataushika upindo wa nguo yake yeye aliye Myahudi; naam, wataushika wakisema, Tutakwenda pamoja nanyi, kwa maana tumesikia kwamba Mungu yu pamoja nanyi.”

Amani ni ufunguo wa mafanikio na ustawi wa mwanadamu kimwili na kiroho, unapokuwa na amani inakusaidia kuwaza na kufikiri maswala ya maendeleo, na kuelekea kwenye ubunifu mkubwa na uzalishaji katika maisha na kazi zetu na ndoa zetu na familia zetu, kila mtu anapaswa kuwa na amani ya ndani na nje na mwanadamu anapokuwa na amani na kuitafuta sana Amani inaleta mchango mkubwa wa ufanisi katika jamii na kutufanya tuishi kwa furaa na amani, watu Fulani wanapoishi katika migogoro yao ni lazima wajue kuwa migogori yao inatuumiza hata sisi tulio nje ya migogoro hiyo kwa sababu hatufurahii kusikia migogoro hiyo upendo haufurahii udhalimu, kila mwenye mgogoro na mtu malizana nao haraka, wako watu wamekufa wakiwa hawajatengeneza maasi na maovu na uharibifu walioufanya kwa wenzao na kuwaumiza, wakafanya shingo zao kuwa ngumu, wakafa wakiwa hawajatafuta Amani!

1Wakorintho 13:4-6 “Upendo huvumilia, hufadhili; upendo hauhusudu; upendo hautakabari; haujivuni;haukosi kuwa na adabu; hautafuti mambo yake; hauoni uchungu; hauhesabu mabaya; haufurahii udhalimu, bali hufurahi pamoja na kweli;”

Na. Rev. Innocent Samuel Kamote.

Mkuu wa wajenzi mwenye hekima!       

0719990897

Hakuna maoni: