Jumamosi, 28 Septemba 2024

Wewe nawe utakuwa kama mmoja wa wapumbavu?


2Samuel 13:11-13 “Naye alipokwisha kuileta karibu naye, ili ale, Amnoni akamkamata, akamwambia, Njoo ulale nami, ndugu yangu. Naye akamjibu, La, sivyo, ndugu yangu, usinitenze nguvu; kwani haifai kutendeka hivi katika Israeli; usitende upumbavu huu. Nami nichukue wapi aibu yangu? Wewe nawe utakuwa kama mmoja wa wapumbavu wa Israeli. Basi, sasa, nakusihi, useme na mfalme; kwa maana hatakukataza kunioa.”      

   



Utangulizi

Mojawapo ya tatizo ambalo limeleta majuto makubwa sana duniani na kuwaingiza wanadamu wengi kwenye changamoto mbalimbali ni pamoja na Upumbavu!, amini usiamini upumbavu umegharimu maisha ya watu wengi sana, na ni kupitia upumbavu aidha wa kwetu wenyewe au wa mtu mwingine, wengi wetu tumejikuta katika matatizo na changamoto zilizogharimu maswala kadhaa katika maisha, na ndio maana unaweza kuona maandiko matakatifu yakisisitiza sana umuhimu wa kuitafuta hekima kwa gharama yoyote ile kwa sababu hekima ni bora sana kuliko madini yoyote yale ya thamani zikiwemo rubi au marijani, Hekima inasimama kama njia ya kutusaidia kuvuka katika dunia hii salama.

Mithali 8:10-11 “Pokea mafundisho yangu, wala si fedha, Na maarifa kuliko dhahabu safi. Maana hekima ni bora kuliko marijani; Wala vyote vinavyotamanika havilingani nayo.”

Kwa msingi huo tunapojifunza somo hili lenye kichwa “Wewe nawe utakuwa kama mmoja wa wapumbavu?” Maana yake ni nini? Maana yake leo tutazungumzia kwa kina na mapana na marefu jinsi tunavyoweza kukwepa kufanya upumbavu tukiwa hapa duniani na hatimaye kuona umuhimu wa kumuomba Mungu na kuifuata njia ya Hekima ili tuweze kufanikiwa katika maisha haya  na yale yajayo, tutajifunza somo hili Wewe nawe utakuwa kama mmoja wa wapumbavu ? kwa kuzingatia vipengele vitatu viafuatavyo:-

·         Maana ya neno Upumbavu

·         Wewe nawe utakuwa kama mmoja wa wapumbavu?

·         Chagua Hekima!

Maana ya neno Upumbavu

Neno upumbavu katika lugha ya kiingereza linaelezewa kwa misamiati mingi sana kama vile fool, lacking of good sense, lacking of good judgement, unwise, stupid, silly, Idiotic, na kadhalika, lakini neno maarufu sana linalotumika katika Biblia hususani agano la kale ambalo limeletwa kwetu kwa lugha ya kiebrania ni neno nãbhãl  neno hilo kimsingi katika tamaduni za kiebrania linachukuliwa kama mtu aliyekosa hekima au mtu aliyepuuzia hekima, mtu asiye na uadilifu, mtu baradhuli, mtu muovu, mtu mbaya, mtu asiyetenda haki, mtu mwenye kuaibisha, mtu anayezungumza pumba, au mtu asiye muungwana, aliekosa uungwana au asiyefunzwa uungwana, mtu wa hila, asiye na akili, au mtu mwenye akili na hekima akifanya jambo la kushangaza kinyume na akili yake au hekima au njia ya Mungu, kwa hiyo katika mtazamo wa kiungu kufanya upumbavu ni kufanya jambo ambali liko kinyume na neno.  

Isaya 32:5-8 “Mpumbavu hataitwa tena mwungwana, wala ayari hatasemwa kwamba ni karimu. Maana mpumbavu atanena yaliyo upumbavu, na moyo wake utafanya maovu, ili kutenda hila na kusema yasiyo kweli juu ya Bwana, ili kuziacha nafsi za watu wenye njaa hazina kitu, na kukikomesha kinywaji chake mwenye kiu. Tena vyombo vyake ayari ni vibaya; hutunga hila mbaya, ili kuwaangamiza wanyonge kwa maneno ya uongo, mtu mhitaji ajaposema maneno yenye haki. Bali mwungwana huwaza mambo ya kiungwana, naye hushika sana mambo ya kiungwana.”

Kwa hiyo katika maandiko, mtu asipofikiri katika kutenda kwake, au akifanya maamuzi mabaya na hata kufikiri vibaya maana yake ametenda kwa upumbavu, na jambo hilo linaweza kutugharimu katika maisha yetu kimwili na kiroho.

2Samuel 24:9-10 “Naye Yoabu akamtolea mfalme jumla ya hesabu ya watu; nao walikuwa wa Israeli mashujaa wenye kufuta panga mia nane elfu; nao wa Yuda walikuwa watu mia tano elfu. Ndipo moyo wake Daudi ukamchoma baada ya kuwahesabu hao watu. Naye Daudi akamwambia Bwana, Nimekosa sana kwa haya niliyoyafanya; lakini sasa, Ee Bwana, nakusihi uuondolee mbali uovu wa mtumishi wako; kwani nimefanya upumbavu kabisa.”        

Kwa hiyo lugha upumbavu katika maandiko inaweza kuwa na upana wa kiharibiko zaidi ya kukosa maarifa, au ukosefu wa ustaarabu na kama mwanadamu hatakuwa makini mtu awaye yote yule, wa ngazi yoyote ile anaweza kujikuta anafanya upumbavu! Bwana ampe neema kila mmoja wetu ili tusiwe miongoni mwa watu watakaofanya upumbavu na kujutia katika maisha yetu, Katika jina la Yesu Kristo ameen!

Wewe nawe utakuwa kama mmoja wa wapumbavu?

Wakati wowote ule tunapofanya jambo ambalo limeagizwa katika neno la Mungu na lina uhusiano na uadilifu hapo tunatenda kwa hekima, na wakati wowote ule tunapofanya jambo ambalo liko kinyume na mapenzi ya Mungu na swala zima la uvunjifu wa uadilifu maana yake tunakuwa tumetenda kwa upumbavu, kwa hiyo upumbavu ni dhambi, upumbavu ni ujinga na upumbavu unaweza kutuweka pabaya, upumbavu unaweza kuyagharimu maisha yetu na ya wengine, na kwa kweli tukiruhusu, wivu, chuki, choyo, ubinafsi, kupenda fedha, kupenda madaraka, kujivuna kutembea kwa kiburi, na kadhalika na hayo yakatawala nafsi zetu ni rahisi sana kujikuta tumefanya upumbavu, kwa hiyo utaweza kuona kuwa dhambi na upumbavu ni mapacha wanaotembea kwa ukaribu sana  na tuwapo duniani  tunapaswa kujihadhari sana tusifanye upumbavu, ili tuweze kuishi kwa Amani.

Katika andiko letu la Msingi, ambalo Roho Mtakatifu Mwalimu mkuu alinipa na ndiko nilikopata kichwa cha ujumbe wa somo hili, tunasoma habari za Amnoni kijana aliyejawa na tamaa na kumpenda dada yake waliozaliwa mama tofauti lakini kwa baba mmoja, kijana huyu alimtamani sana dada yake na kiasi ambacho aliandaa njama za kutaka kumbaka, dada huyu alimshauri vizuri kwamba kama unanipenda unaweza kuzungumza na mfalme baba yao na hatakuzuia kunioa, lakini yeye akizidiwa na tamaa aliendelea na mpango wake wa kutaka kumbaka, dada yake aliyeonekana kuwa na busara sana alimshauri kuwa kwa kutumia njia anayotaka kuitumia atakuwa kama mojawapo ya wapumbavu katika Israel, yaani licha ya kuwa amefanya dhambi lakini atakuwa amefanya upumbavu, hii maana yake ni nini? wakati wote tunapoacha kutumia busara katika jambo lolote lile na tukaachia hisia zetu na tamaa ya mioyo yetu ituongoze maana yake au kinyume chake tunachagua njia ya kipumbavu na swali hili litatuhusu wewe nawe utakuwa kama mmoja wa wapumbavu?, maandiko matakatifu yamejaa mifano mingi ya watu waliotenda kwa upumbavu ambayo sisi hatupaswi kuiigia, kwani yaliandikwa kwa kusudi la kutupa hekima sisi tunaoishi miisho ya zamani hizi ili tusifanye upumbavu, kwa mfano:-

1.       Ukiwaza moyoni kuwa hakuna Mungu – Maandiko yanaonya kuwa sio kusema tu lakini mtu awaye yote ambaye anawaza moyoni mwake kuwa hakuna Mungu kibiblia huyo ni mpumbavu, hajishughulishi kumtafuta Mungu, haamini kama Mungu yupo, huyo ni mtenda maovu, awaye yote yule ambaye anaishi kana kwamba hakuna Mungu naye ni mpumbavu, wote wanaoishi kwa ukaidi wakikataa miongozo ya Mungu, wakilikataa neno la Mungu, wakiwa hawamtafuti Mungu na wanaishi sawa tu mawazo yao hao wanakuwa wamekengeuka na jumla yaw azo la kimungu kwao katika maandiko ni kuwa wamepumbazika.

 

Zaburi 14:1-3 “Mpumbavu amesema moyoni, Hakuna Mungu; Wameharibu matendo yao na kuyafanya chukizo, Hakuna atendaye mema. Toka mbinguni Bwana aliwachungulia wanadamu, Aone kama yuko mtu mwenye akili, Amtafutaye Mungu. Wote wamepotoka, wameoza wote pamoja, Hakuna atendaye mema, La! Hata mmoja.”

 

Zaburi 53:1-3 “Mpumbavu amesema moyoni, Hakuna Mungu; Wametenda uovu wa ufisadi na kuchukiza, Hakuna atendaye mema. Toka mbinguni MUNGU aliwachungulia wanadamu, Aone kama yuko mtu mwenye akili, Amtafutaye Mungu.Kila mtu amepotoka, wameoza wote pamoja, Hakuna atendaye mema, La! Hata mmoja.”

 

2.       Anayeshauri mtu amwache Mungu – Wako watu ambao katika namna ya kushangaza sana wanaweza kukushauri umwache Mungu, au utafute msaada kwa miungu mingine kwa sababu ya changamoto unazozipitia na misimamo yako katika kumuamini Mungu mtu anayefanya hivyo au kutoa ushauri wa namna hiyo katika maandiko anatajwa kama mtu anayezungumza upumbavu au pumba. Aidha mtu awaye yeto akikubali kuyategemea mawazo yake na njia zake au njia za kibinadamu huyu naye anatenda kwa upumbavu

 

Ayubu 2:7-10 “Basi Shetani akatoka mbele za uso wa Bwana, akampiga Ayubu na majipu mabaya tangu wayo wa mguu hata utosi wa kichwa. Naye akashika kigae cha kujikunia; akaketi majivuni. Ndipo mkewe akamwambia, Je! Wewe hata sasa washikamana na utimilifu wako? Umkufuru Mungu, ukafe. Lakini yeye akamwambia, Wewe wanena kama mmoja wa hao wanawake wapumbavu anenavyo. Je! Tupate mema mkononi mwa Mungu, nasi tusipate na mabaya? Katika mambo hayo yote Ayubu hakufanya dhambi kwa midomo yake.”  

 

3.       Kuondoka bila kuaga – Umekaa na mtu kwa muda mrefu katika maisha yako, au mahali ambapo ulikuwa unafanya kazi, alafu ukaamua kuondoka bila kuaga, au kutokumuaga baba yako wa kiroho, na kuamua kutoroka, bila kuagana kwa Amani na kubarikiana tendo hilo kadhalika linaweza kuwa sio dhambi lakini sio la kiungwana  wala kistaarabu kwa hivyo katika maandiko ukilifanya unahesabika kuwa umefanya upumbavu.

 

Mwanzo 31:26-28 “Labani akamwambia Yakobo, Umefanya nini? Umenihadaa, ukawachukua binti zangu kama mateka waliotwaliwa kwa upanga. Mbona umekimbia kwa siri ukanihadaa, wala hukuniambia, nipate kuagana nawe uende zako kwa furaha, na nyimbo, na ngoma, na kinubi? Wala hukuniacha niwabusu wanangu, na binti zangu; basi umetenda upumbavu.”

 

4.       Kulala na binti ya watu kabla ya kumchumbia au kumuoa – kimaandiko unapolala na binti ya watu na ukambikiri, kabla ya kumuoa kwa madai kuwa utamuoa baadaye jambo la namna hii ni la kipumbavu katika tamaduni za kimaandiko na Israel. Huwezi kuishi kama mwana ndoa kabla ya ndoa kwa kufanya hivyo unajidhihirisha namna ambavyo umekosa adabu, umekosa heshima, umekosa maarifa huna hekima na umefanya upumbavu.

 

Mwanzo 34:1-7 “Basi Dina, binti Lea, ambaye Lea alimzalia Yakobo, akatoka kuwaona binti za nchi. Shekemu, mwana wa Hamori, Mhivi, mkuu wa nchi, akamwona akamtwaa, akalala naye, akambikiri. Moyo wake ukaambatana na Dina binti Yakobo, akampenda huyu msichana, akasema na huyu msichana kwa maneno mazuri. Shekemu akamwambia Hamori, babaye, akasema, Unipatie msichana huyu awe mke wangu. Basi Yakobo akasikia ya kwamba amembikiri Dina, binti yake. Na wanawe walikuwako pamoja na wanyama wake nyikani. Yakobo akanyamaza, hata walipokuja. Akatoka Hamori, babaye Shekemu, kumwendea Yakobo, aseme naye. Wanawe Yakobo waliposikia hayo, wakaja kutoka nyikani; nao wakasikitika sana, wakakasirika mno, kwa sababu amefanya upumbavu katika Israeli kwa kulala na binti Yakobo, neno lisilojuzu kutendeka.”           

 

5.       Kumdhalilisha mwanamke – tendo la mtu kumuoa mwanamke aliye bikira, kisha akafika ndani na ukamchukia kisha kumsingizia kuwa eti hakuwa na ubikira tendo la kumdhalilisha na kumuaibisha mwanamke katika Israel na katika swala zima la uadilifu ni kutenda upumbavu.

 

Kumbukumbu 22:13-21 “Mtu akitwaa mke, akamwingilia na kumchukia, kisha akamshitaki mambo ya aibu kumzushia jina baya, akasema, Nimemtwaa mwanamke huyu, nami nilipomkaribia sikuona kwake alama za ubikira; ndipo babaye yule kijana na mamaye watakapotwaa alama za yule kijana za ubikira, wawatolee wazee wa mji langoni; na baba yake yule kijana awaambie wazee, Mwanamume huyu nilimpa binti yangu awe mkewe, naye amchukia; angalieni, amemwekea mambo ya aibu, asema, Sikuona kwa binti yako alama za ubikira, nazo hizi ndizo alama za binti yangu za ubikira. Na wayakunjue yale mavazi mbele ya wazee wa mji. Basi wazee wa mji ule na wamtwae yule mtu mume na kumrudi, wamtoze shekeli mia za fedha, wampe babaye yule kijana, kwa kuwa amemzulia jina baya mwanamwali wa Israeli; naye awe mkewe; hana ruhusa ya kumwacha siku zake zote. Lakini likiwa ni kweli neno hili, la kutoonekana kwake yule kijana alama za ubikira; na wamtoe nje yule kijana mlangoni pa nyumba ya baba yake, na waume wa mji wake wampige kwa mawe hata afe; kwa vile alivyofanya upumbavu katika Israeli, kwa kufanya ukahaba katika nyumba ya baba yake; ndivyo utakavyoondoa uovu katikati yako.”

               

6.       Awaye yote anayeiba – Maandiko matakatifu yanaagiza kuwa tusiibe, lakini sio hivyo tu kila mmoja anaagizwa kuyatii maagizo ya Bwana na kulishika agano lake, kufanya jambo kinyume na hayo ni kufanya upumbavu, mtu anayeiba ni mpumbavu, amechagua njia isiyo ya kiungwana.

 

Yoshua 7:11-15 “Israeli wamefanya dhambi, naam, wamelivunja agano langu nililowaagiza; naam, wametwaa baadhi ya vitu vilivyowekwa wakfu; tena wameiba, tena wameficha na kuvitia pamoja na vitu vyao wenyewe. Ndiposa wana wa Israeli hawawezi kusimama mbele ya adui zao; wakawapa visogo adui zao, kwa sababu wamelaaniwa; mimi sitakuwa pamoja nanyi tena, msipokiharibu kitu kile mlicho nacho kilichowekwa wakfu. Haya! Inuka, uwatakase watu, ukaseme, Jitakaseni, mwe tayari kesho; maana Bwana, Mungu wa Israeli, asema hivi; Kitu kilichowekwa wakfu kiko katikati yako, Ee Israeli; huwezi kusimama mbele ya adui zako, hata mtakapokiondoa kile mlicho nacho kilichowekwa wakfu. Basi asubuhi mtaletwa karibu nami kabila kwa kabila; kisha itakuwa ya kwamba kabila ile atakayoitwaa Bwana itakaribia jamaa kwa jamaa; na jamaa ile atakayoitwaa Bwana itakaribia nyumba kwa nyumba; na nyumba ile atakayoitwaa Bwana itakaribia mtu kwa mtu. Tena itakuwa ya kwamba yeye atakayetwaliwa, naye anacho kitu kile kilichowekwa wakfu, atateketezwa kwa moto, yeye na vitu vyote alivyo navyo; kwa sababu amelivunja agano la Bwana, na kwa sababu ametenda upumbavu katika Israeli.”

 

7.       Kumbaka mwanamke -  Kumbaka mwanamke na kumuingilia kinyume cha maumbile, sio tu kuwa ni dhambi, lakini vilevie ni upumbavu, katika jamii, jambo hilo ni uovu ambao sio tu utakugharimu kufunguliwa mashitaka na kufungwa lakini kwa Mungu ni dhambi na ni uovu katika jamii.

 

Waamuzi 20:4-6 “Huyo Mlawi, huyo mume wa mwanamke aliyeuawa, akajibu na kusema, Mimi nilifikilia Gibea ulio wa Benyamini mimi na suria yangu, ili tulale. Nao watu waume wa Gibea wakaniondokea, na kuizingira hiyo nyumba pande zote juu yangu wakati wa usiku; walidhani kuniua, na suria wangu wakamtenza nguvu, hata amekufa.Basi nikamtwaa huyo suria yangu, na kumkata vipande, na kumpeleka katika nchi yote ya urithi wa Israeli; kwa sababu wametenda maovu makuu na upumbavu katika Israeli.”

 

8.       Tamaa na kutaka kulawiti ni upumbavu – jamii inapokuwa na watu ambao wanaona kuwa mapenzi ya jinsia moja kama jambo la kawaida maana yake jamii hiyo imepumbazika, usagaji ni upumbavu, ulawiti ni upumbavu, usagaji ni upumbavu, ni kukosa akili ni kukosa hekima kwa hiyo ukiiangalia dunia ya leo na swala zima la maovu yanayohusiana na ulawiti na tamaa ya aina hiyo utaweza kuwa na picha halisi kuwa watu hata pamoja na kuwa na elimu kubwa hivyo na marifa kuongezeka, dunia imekuwa na wapumbavu wengi sana.

 

Waamuzi 19:23-25 “Naye mtu mwenye nyumba akawatokea hapo nje, na kuwaambia, La, sivyo, ndugu zangu nawasihi msifanye uovu jinsi hii; kwa kuwa mtu huyu ameingia ndani ya nyumba yangu, msifanye upumbavu huu. Tazama, binti yangu yupo hapa, ni mwanamwali, na suria wake huyo mtu; nitawaleta hapa nje sasa nanyi watwezeni, na kuwatenda hayo myaonayo kuwa ni mema; lakini mtu huyu msimtende jambo la upumbavu namna hii. Lakini hao watu hawakukubali kumsikia; basi mtu huyo akamshika suria wake, na kumleta nje kwao; nao wakamjua, na kumtenda uovu usiku kucha hata asubuhi kisha kulipoanza kupambauka wakamwacha aende zake.”

 

Warumi 1:21-28 “kwa sababu, walipomjua Mungu hawakumtukuza kama ndiye Mungu wala kumshukuru; bali walipotea katika uzushi wao, na mioyo yao yenye ujinga ikatiwa giza. Wakijinena kuwa wenye hekima walipumbazika; wakaubadili utukufu wa Mungu asiye na uharibifu kwa mfano wa sura ya binadamu aliye na uharibifu, na ya ndege, na ya wanyama, na ya vitambaavyo. Kwa ajili ya hayo Mungu aliwaacha katika tamaa za mioyo yao, waufuate uchafu, hata wakavunjiana heshima miili yao. Kwa maana waliibadili kweli ya Mungu kuwa uongo, wakakisujudia kiumbe na kukiabudu badala ya Muumba anayehimidiwa milele. Amina. Hivyo Mungu aliwaacha wafuate tamaa zao za aibu, hata wanawake wakabadili matumizi ya asili kwa matumizi yasiyo ya asili; wanaume nao vivyo hivyo waliyaacha matumizi ya mke, ya asili, wakawakiana tamaa, wanaume wakiyatenda yasiyopasa, wakapata nafsini mwao malipo ya upotevu wao yaliyo haki yao.Na kama walivyokataa kuwa na Mungu katika fahamu zao, Mungu aliwaacha wafuate akili zao zisizofaa, wayafanye yasiyowapasa.”                   

 

9.       Kuropoka – nadhani umewahi kuishi na watu wanaoropoka, na utakuwa unajua madhara ya kuropoka, kuropoka ni kuzungumza kitu bila kufikiri, wako watu yaani kitakachomjia kichwani tu anakitekeleza kwa kusema au kuandika sms isiyofaa, unaweza kutuma ujumbe usiofaa kwa mke wa mtu, mume wa mtu, unaweza kuropoka mambo ya watu au siri za watu, au kutokwa na maneno yasiyo na maana kama mtu hana nidhamu katika kuzungumza kwake maana yake anashindwa kuudhibiti ulimi wake naye anaitwa mpumbavu

 

Mithali 14:3 “Katika kinywa cha mpumbavu mna fimbo ya kiburi, Bali midomo ya wenye hekima huwahifadhi.”  

 

Mithali 12:15-16 “Njia ya mpumbavu imenyoka machoni pake mwenyewe; Bali yeye aliye na hekima husikiliza shauri. Ghadhabu ya mpumbavu hujulika mara; Bali mtu mwerevu husitiri aibu.”

 

10.   Kufanya dhambi – Kufanya dhambi ya aina yoyote ile kibiblia ilihesabika kuwa ni kufanya upumbavu, kwani kila dhambi licha ya kuwa uko msamaha wa Mungu na rehema zake lakini kwa kuwa Mungu ni mwenye haki wakati mwingine matokeo ya dhambi yanaweza kuendeleza madhara makubwa nje ya msamaha wa Mungu, mfano ukifanya uasherati ukapata mimba, na ukatubu kwa uasherati ule utasamehewa lakini mimba haitayeyuka kwa hiyo ulipaswa kufikiri kabla ya kutenda na kwa kutokufikiri umefanya upumbavu. Na au ukapata ukimwi, rehema za Mungu zinaweza kuwepo lakini na virusi vinaendelea kuwepo kwa sababu ulifanya upumbavu, hukutoa nafasi ya kufikiri kwa kina madhara unayoweza kuyapata. Kwa hiyo ni muhimu kukumbuka ya kuwa dhambi ina madhara yake na madhara yake ni mabaya sana katika maisha ya watu wote

 

Zaburi 38:3-5 “Hamna uzima katika mwili wangu Kwa sababu ya ghadhabu yako. Wala hamna amani mifupani mwangu Kwa sababu ya hatia zangu. Maana dhambi zangu zimenifunikiza kichwa, Kama mzigo mzito zimenilemea mno. Jeraha zangu zinanuka, zimeoza, Kwa sababu ya upumbavu wangu.”

 

Zaburi 69:3-5 “Nimechoka kwa kulia kwangu, Koo yangu imekauka. Macho yangu yamedhoofu Kwa kumngoja Mungu wangu. Wanaonichukia bure ni wengi Kuliko nywele za kichwa changu. Watakao kunikatilia mbali wamekuwa hodari, Adui zangu kwa sababu isiyo kweli. Hata mimi nalilipishwa kwa nguvu Vitu nisivyovichukua. Ee Mungu, unajua upumbavu wangu, Wala hukufichwa dhambi yangu.”

 

11.   Ukiruhusu hasira kukutawala – wako watu ambao kupitia hasira wamefanya mambo ya kijinga na kipumbavu na baadaye kujilaumu au kupata majuto, maandiko yanatutaka kujidhibiti, kujitia nidhamu, badala ya kujisifia kuwa wewe una hasira, hakikisha unajinidhamu kushindwa kufanya hivyo ni kuruhusu upumbavu.

 

Muhubiri 7:4-9 “Moyo wake mwenye hekima umo nyumbani mwa matanga, bali moyo wake mpumbavu umo nyumbani mwa furaha. Heri kusikia laumu ya wenye hekima, Kuliko mtu kusikia wimbo wa wapumbavu; Maana kama mlio wa miiba chini ya sufuria, Ndivyo kilivyo kicheko cha mpumbavu. Hayo nayo ni ubatili. Kweli jeuri humpumbaza mwenye hekima, Na rushwa huuharibu ufahamu. Heri mwisho wa neno kuliko mwanzo wake, Na mvumilivu rohoni kuliko mwenye roho ya kiburi. Usifanye haraka kukasirika rohoni mwako, Maana hasira hukaa kifuani mwa wapumbavu.”

 

12.   Kumtendea maovu mtu ambaye hana nia mbaya na wewe – wako watu wengine kwa sababu ya wivu tu wenye uchungu wanaweza kukutendea mabaya, au wanaweza kukusudia kutenda mabaya kwa watu ambao hawana nia wala wazo la kuwadhuru, kufanya jambo la namna hiyo ni machukizo sio kwa Mungu tu lakini ni upumbavu, kutafuta na kutaka kumdhuru mtu ambaye hana mpango wala nia ya kukudhuru.

 

1Samuel 26:18-21. “Akasema, Bwana wangu ananiwinda mimi mtumishi wake kwa sababu gani? Nimefanya nini mimi? Ni uovu gani nilio nao mkononi mwangu? Basi sasa, nakusihi, bwana wangu, mfalme, na asikie maneno ya mtumishi wake. Ikiwa ni Bwana aliyekuondokesha juu yangu, na akubali sadaka; bali ikiwa ni wanadamu, na walaaniwe mbele za Bwana; kwa sababu wamenifukuza leo, nisishikamane na urithi wa Bwana, wakisema, Enenda, katumikie miungu mingine.Basi sasa, isianguke damu yangu chini mbali na uso wa Bwana; maana mfalme wa Israeli ametoka ili kutafuta uhai wangu, kama vile mtu awindavyo kware mlimani.Ndipo Sauli akasema, Nimekosa; rudi, Daudi, mwanangu; maana sitakudhuru tena, kwa kuwa maisha yangu yalikuwa na thamani machoni pako leo; angalia, nimetenda upumbavu, nimekosa sana.”     

 

13.   Mtu anayefikiria maovu na mwenye mizaha - Maandiko yanataja vitu kadhaa vinavyomchukiza Mungu, ikiwa ni pamoja na moyo uwazao mabaya, yaani maswala hayo ni machukizo kwa Mungu, maana yake kule kufikiri na kuwaza namna ya kufanya maovu, ni kufikiri na kufanya dhambi hayo yanawekwa katika kundi moja la machukizo kwa Mungu, ambayo kimsingi nayo yanaitwa upumbavu katika maandiko kwa sababu moyoni ndiko chanzo cha kila kitu kibaya kwa hiyo kufikiri au kuwaza maovu ni kuwaza upumbavu na zaidi sana ikiwa ni pamoja na mizaha, kwa hiyo kila mmoja wetu ajichunge fikira zake na kujihadhari za mizaha.  

 

Mithali 6:16-19 “Kuna vitu sita anavyovichukia Bwana; Naam, viko saba vilivyo chukizo kwake. Macho ya kiburi, ulimi wa uongo, Na mikono imwagayo damu isiyo na hatia; Moyo uwazao mawazo mabaya; Miguu iliyo myepesi kukimbilia maovu;Shahidi wa uongo asemaye uongo; Naye apandaye mbegu za fitina kati ya ndugu.”

 

Mithali 24:9 “Fikira za mpumbavu ni dhambi, Na mwenye mzaha huwachukiza watu.”

 

14.   Mtu anayelipa maovu badala ya mema – kwa maana nyingine ni watu wasio na shukurani, wako watu ambao unaweza kuwatendea mema na kisha ukahitaji fadhili ndogo tu kutoka kwao lakini wakakulipa mabaya badala ya mema mfano wa aina hii ya upumbavu ndio uliofanywa na mtu mwenye kuitwa nabali ambayo ndio tafasiri ya somo hili Nabali maana yake mpumbavu ambaye alioa mwanamke muungwana au mwenye akili.

 

1Samuel 25:2-26 “Na huko Maoni kulikuwa na mtu mmoja, ambaye alikuwa na mali yake katika Karmeli; naye yule mtu alikuwa mkuu sana, mwenye kondoo elfu tatu na mbuzi elfu; naye alikuwa akiwakata manyoya kondoo zake huko Karmeli. Na jina la mtu huyo aliitwa Nabali; na jina la mkewe aliitwa Abigaili, na huyo mwanamke alikuwa mwenye akili njema, mzuri wa uso; bali yule mwanamume alikuwa hana adabu, tena mwovu katika matendo yake; naye alikuwa wa mbari ya Kalebu. Basi Daudi akasikia huko nyikani ya kuwa Nabali alikuwa katika kuwakata manyoya kondoo zake. Daudi akatuma vijana kumi, Daudi naye akawaambia hao vijana, Kweeni mwende Karmeli, na kumwendea huyu Nabali ili mnisalimie; na hivi ndivyo mtakavyomwambia huyu aishiye salama, Amani na iwe kwako, na amani nyumbani mwako, na amani kwao wote ulio nao. Nami sasa nimesikia ya kuwa una watu wanaokata manyoya kondoo zako; haya! Wachungaji wako wamekuwa pamoja nasi, wala hatukuwadhuru, wala hawakukosa kitu wakati wote walipokuwako huko Karmeli. Waulize vijana wako, nao watakuambia; basi na wakubaliwe vijana hawa machoni pako; maana tumekujia katika siku ya heri; uwape, nakusihi, cho chote kitakachokujia mkononi, uwape watumwa wako na mwanao Daudi. Basi walipofika vijana wake Daudi, wakamwambia Nabali sawasawa na maneno hayo yote kwa jina la Daudi, kisha wakanyamaza. Naye Nabali akawajibu wale watumishi wa Daudi, akasema, Huyu Daudi ni nani? Na mwana wa Yese ni nani? Siku hizi kuna watumwa wengi wanaomtoroka kila mtu bwana wake! Basi mimi je! Nitwae mkate wangu, na maji yangu, na machinjo yangu niliyowachinjia hao watu wangu wakatao manyoya kondoo zangu, na kuwapa watu ambao siwajui wametoka wapi? Basi vijana wake Daudi wakageuka, wakaenda zao, wakarudi, nao wakaja wakamwambia sawasawa na maneno hayo yote. Kisha Daudi akawaambia watu wake, Haya! Jifungeni kila mtu upanga wake. Nao wakajifunga kila mtu upanga wake; Daudi naye akajifunga upanga wake; nao wakapanda nyuma yake Daudi, wapata kama watu mia nne; na watu mia mbili wakakaa na vyombo vyao.Lakini kijana mmojawapo alimpasha habari Abigaili, mkewe Nabali, kasema, Tazama, Daudi alituma wajumbe kutoka nyikani waje ili kumsalimu bwana wetu, naye akawatukana. Walakini watu hawa walitutendea mema sana, wala hatukupata dhara, wala sisi hatukupotewa na kitu cho chote, wakati wote tulipofuatana nao, tulipokuwako mavueni; watu hao walikuwa boma kwetu usiku na mchana, wakati wote tulipokuwa nao tukiwachunga kondoo. Basi sasa ujue na kufikiri utakayotenda; kwa sababu yamekusudiwa mabaya juu ya bwana wetu, na juu ya nyumba yake yote; kwa kuwa yeye ni mtu asiyefaa kabisa, hata mtu hawezi kusema naye. Ndipo Abigaili akafanya haraka, akatwaa mikate mia mbili, na viriba viwili vya divai, na kondoo watano waliofanyizwa tayari, na vipimo vitano vya bisi, na vishada mia vya zabibu, na mikate ya tini mia mbili; akavipakia vitu hivi juu ya punda. Akawaambia vijana wake, Haya! Tangulieni mbele yangu; angalieni, mimi nawafuata. Ila hakumwambia mumewe, Nabali. Ikawa, alipokuwa amepanda punda wake, na kutelemka penye sitara ya mlima, tazama, Daudi na watu wake walikuwa wakishuka kumkabili; naye akawakuta. Basi Daudi alikuwa amesema, Hakika ni bure nilivyokuwa nikilinda nyikani yote aliyo nayo mtu huyu, asipotewe na kitu cho chote cha mali yake yote; naye amenilipa mabaya badala ya mema. Mungu naye awafanyie hivyo adui za Daudi, na kuzidi, nikimwachia katika wote walio wake hata mtoto mume mmoja, kutakapopambazuka asubuhi. Ndipo hapo Abigaili alipomwona Daudi, alifanya haraka kushuka juu ya punda wake, akamwangukia Daudi kifulifuli, akainama mpaka nchi. Akamwangukia miguuni pake, akasema, Juu yangu, bwana wangu, juu yangu mimi na uwe uovu; tafadhali mjakazi wako na anene masikioni mwako, nawe uyasikilize maneno ya mjakazi wako. Nakusihi, bwana wangu, wewe usimwangalie huyu mtu asiyefaa, yaani, Nabali; kwa maana kama lilivyo jina lake ndivyo alivyo yeye; jina lake ndilo Nabali, na upumbavu anao; lakini mimi, mjakazi wako, sikuwaona hao vijana wa bwana wangu aliowatuma. Basi sasa, bwana wangu, aishivyo Bwana, na iishivyo nafsi yako, kwa kuwa Bwana amekuzuia usimwage damu, tena usijilipize kisasi mkono wako mwenyewe, basi sasa adui zako, na hao wamtakiao bwana wangu mabaya, wawe kama Nabali.”

 

15.   Mwanamke asiye na hekima – Biblia aidha pia ina maonyo mengi kuhusu mwanamke mcha Mungu, na mwenye hekima kuwa ni mwanamke anayeweza kusimamia nyumba yake vizuri, na maandiko yanaonyesha kuwa kama mwanamke hamchi Mungu nyumba yake haiwezi kusimama mwanamke asiye mcha Mungu anaweza kuhesabika kama mkaidi, asiyetaka kumtii Mumewe, hafundishiki, mbishi, mbinafsi, anayetawala nyumba, mchoyo kwa tendo la ndoa na anayeamua kumkomoa mumewe kwa tendo hilo, mvivu wa ibada, hajishushi, mumewe akipanda naye anapanda juu zaidi, anayependa usingizi, Mmbeya, hafanyi kazi kwa mikono yake mwenyewe, na majukumu ya mke anayapuuzia na kupenda starehe nyingine utaongezea mwenyewe mwanamke wa aina hiyo ndiye anayefikiriwa kuwa hana hekima na hivyo maandiko yanamuita mpumbavu.

 

Mithali 14:1-2 “Kila mwanamke aliye na hekima hujenga nyumba yake; Bali aliye mpumbavu huibomoa kwa mikono yake mwenyewe. Yeye aendaye kwa unyofu wake humcha Bwana; Bali aliye mkaidi katika njia zake humdharau.”

 

Mithali 9:13-17 “Mwanamke mpumbavu hupiga kelele, Ni mjinga, hajui kitu.Hukaa mlangoni pa nyumba yake, Juu ya kiti mahali pa mjini palipoinuka, Apate kuwaita wapitao njiani, Waendao moja kwa moja katika njia zao. Kila aliye mjinga na aingie humu. Tena amwambia mtu aliyepungukiwa na akili, Maji yaliyoibiwa ni matamu, Na mkate ulioliwa kwa siri hupendeza.”

 

Mithali 21:9 “Ni afadhali kukaa katika pembe ya darini, Kuliko katika nyumba pana pamoja na mwanamke mgomvi.”

               

Mithali 21:19 “Ni afadhali kukaa katika nchi ya nyika; Kuliko na mwanamke mgomvi, mchokozi.”

               

Mithali 25:24 “Ni afadhali kukaa katika pembe ya darini, Kuliko katika nyumba pana pamoja na mwanamke mgomvi.”

 

16.   Kutokumjua Mungu wala njia zake  Watu wanaweza kuwa na maarifa ya aina nyingine mfano maarifa ya kupanga ubaya, kufanya maovu, kutekeleza majungu, kuharibu mahusiano, lakini hawana maarifa wala akili ya kumtafuta Mungu, ziko nguvu za uovu ambazo watu wanazifanya ambazo kama zingeelekezwa katika kumtafuta Mungu na kuongeza maarifa ya kumjua Mungu watu wangekuwa mbali sana

 

Yeremia 4:22 “Kwa maana watu wangu ni wapumbavu, hawanijui; ni watoto waliopungukiwa na akili, wala hawana ufahamu; ni wenye akili katika kutenda mabaya, bali katika kutenda mema hawana maarifa.”

 

17.   Wanaoamini Manabii wa uongo – Wako manabii ambao kazi yao kubwa ni kuzungumza maneno ya kufariji watu, ilihali wakati mwingine suluhu ya uponyaji wa watu hao ni kuwaambia tu watubu dhambi zao, ziko changamoto nyingi sana duniani zinazosababishwa na dhambi kuliko hata wachawi na laana za ukoo, wakati mwingine mtu akisamehewa dhambi zake na uponyaji wake unakuja kama neno lake lisemavyo, akusamehe maovu yako yote, akuponya magonjwa yako yote, waambie watu kosa lao badala ya kuona maono ya ubatili na upumbavu, manabii wa uongo huona maono ya kipumbavu na hivyo kuzuia kuponywa kwako.

 

Maombolezo 2:13-14 “Nikushuhudie nini? Nikufananishe na nini, Ee Binti Yerusalemu? Nikusawazishe na nini, nipate kukufariji, Ee bikira binti Sayuni? Kwa maana uvunjifu wako ni mkuu kama bahari, Ni nani awezaye kukuponya? Manabii wako wameona maono kwa ajili yako Ya ubatili na upumbavu Wala hawakufunua uovu wako, Wapate kurudisha kufungwa kwako; Bali wameona mabashiri ya ubatili kwa ajili yako Na sababu za kuhamishwa.”                

 

18.   Kutokulifanyia kazi neno la Mungu – kama watu wengi tungekuwa tunalitii neno la Mungu tungekuwa na mafanikio makubwa sana na ustawi mkubwa sana katika maswala yote ya mwili na roho lakini kwa bahati mbaya sana kulitii neno la Mungu limekuwa jambo gumu kwa kizazi hiki hata kama watu wanatii wengi huchagua maswala kadhaa ya kuyatii lakini neno la Mungu linatukumbusha kuyatii maagizo yote na kuyafanyia kazi maneno ya Mungu.

 

Yakobo 1:22-24 “Lakini iweni watendaji wa neno, wala si wasikiaji tu, hali mkijidanganya nafsi zenu.Kwa sababu mtu akiwa ni msikiaji wa neno tu, wala si mtendaji, mtu huyo ni kama mtu anayejiangalia uso wake katika kioo. Maana hujiangalia, kisha huenda zake, mara akasahau jinsi alivyo.”

 

Mathayo 7:24-27 “Basi kila asikiaye hayo maneno yangu, na kuyafanya, atafananishwa na mtu mwenye akili, aliyejenga nyumba yake juu ya mwamba; mvua ikanyesha, mafuriko yakaja, pepo zikavuma, zikaipiga nyumba ile, isianguke; kwa maana misingi yake imewekwa juu ya mwamba. Na kila asikiaye hayo maneno yangu asiyafanye, atafananishwa na mtu mpumbavu, aliyejenga nyumba yake juu ya mchanga; mvua ikanyesha, mafuriko yakaja, pepo zikavuma, zikaipiga nyumba ile, ikaanguka; nalo anguko lake likawa kubwa.”

 

19.   Kujilinganisha na wengine – Katika maisha haya Mungu amemuumba kila mwanadamu akiwa na baraka tofauti na karama na vipawa tofauti, kwa hiyo kimaandiko mwanadamua anyejilinganisha na mwingine au kuipima nafsi yake akiilinganisha nay a mtu mwingine mtu huyo hana akili na ni mpumbavu, kwa mujibu wa maandiko, hatupaswi kamwe kujilinganisha na wengine kwa sababu kila mwanadamu Mungu amemuumba kwa namna na jinsi ya aina yake kwa uhodari mkubwa!

 

2Wakorintho 10:11-18 “Mtu kama huyo na afikiri hivi, ya kwamba jinsi tulivyo kwa maneno katika nyaraka tusipokuwapo, ndivyo tulivyo kwa matendo tukiwapo. Kwa kuwa hatuthubutu kujihesabu pamoja na baadhi yao wanaojisifu wenyewe, wala kujilinganisha nao; bali wao wenyewe wakijipima nafsi zao na nafsi zao, na wakijilinganisha nafsi zao na nafsi zao, hawana akili. Lakini sisi hatutajisifu zaidi ya kadiri yetu; bali kwa kadiri ya kipimo tulichopimiwa na Mungu, yaani, kadiri ya kufika hata kwenu. Maana hatujitanui nafsi zetu kupita kadiri yetu, kana kwamba hatuwafikii ninyi; kwa sababu tulitangulia kufika mpaka kwenu katika injili ya Kristo; wala hatujisifu zaidi ya kadiri yetu, yaani, katika taabu za watu wengine; bali tukiwa na tumaini ya kwamba, imani yenu ikuapo, tutakuzwa kwenu kwa kadiri ya kipimo chetu, na kupata ziada; hata kuihubiri Injili katika nchi zilizo mbele kupita nchi zenu; tusijisifu katika kipimo cha mtu mwingine kwa mambo yaliyokwisha kutengenezwa. Lakini, Yeye ajisifuye, na ajisifu katika Bwana. Maana mtu mwenye kukubaliwa si yeye ajisifuye, bali yeye asifiwaye na Bwana.”

 

20.   Kutokujitayarisha kwa Mungu -  watu wote duniani wanapaswa kujiandaa kwaajili ya kukutana na Mungu, na kujiandaa kwaajili ya ujio wa Bwana wetu Yesu Kristo mara ya pili duniani, na kunyakuliwa kwa kanisa, kuishi maisha ya vuguvugu na kujidanganya kunaweza kuja kutuletea majuto na kilio na kusaga meno, Yesu mara kadhaa alisisitiza jamii kujiandaa kwaajili ya Mungu na awaye yote ambaye atakosa mbingu atakuwa amekosa kwaajili ya upumbavu, Bwana amtunze kila mmoja wetu asiikose mbingu katika jina la Yesu Kristo.

 

Luka 12:16-21 “Akawaambia mithali, akisema, Shamba la mtu mmoja tajiri lilikuwa limezaa sana; akaanza kuwaza moyoni mwake, akisema, Nifanyeje? Maana sina pa kuyaweka akiba mavuno yangu.  Akasema, Nitafanya hivi; nitazivunja ghala zangu, nijenge nyingine kubwa zaidi, na humo nitaweka nafaka yangu yote na vitu vyangu. Kisha, nitajiambia, Ee nafsi yangu, una vitu vyema vingi ulivyojiwekea akiba kwa miaka mingi; pumzika basi, ule, unywe, ufurahi. Lakini Mungu akamwambia, Mpumbavu wewe, usiku huu wa leo wanataka roho yako! Na vitu ulivyojiwekea tayari vitakuwa vya nani? Ndivyo alivyo mtu ajiwekeaye nafsi yake akiba, asijitajirishe kwa Mungu.”

 

Mathayo 25:1-13 “Ndipo ufalme wa mbinguni utakapofanana na wanawali kumi, waliotwaa taa zao, wakatoka kwenda kumlaki bwana arusi. Watano wao walikuwa wapumbavu, na watano wenye busara. Wale waliokuwa wapumbavu walizitwaa taa zao, wasitwae na mafuta pamoja nao; bali wale wenye busara walitwaa mafuta katika vyombo vyao pamoja na taa zao. Hata bwana arusi alipokawia, wote wakasinzia wakalala usingizi. Lakini usiku wa manane, pakawa na kelele, Haya, bwana arusi; tokeni mwende kumlaki. Mara wakaondoka wanawali wale wote, wakazitengeneza taa zao. Wale wapumbavu wakawaambia wenye busara, Tupeni mafuta yenu kidogo; maana taa zetu zinazimika. Lakini wale wenye busara wakawajibu, wakisema, Sivyo; hayatatutosha sisi na ninyi; afadhali shikeni njia mwende kwa wauzao, mkajinunulie.Na hao walipokuwa wakienda kununua, bwana arusi akaja, nao waliokuwa tayari wakaingia pamoja naye arusini; mlango ukafungwa.Halafu wakaja na wale wanawali wengine, wakasema, Bwana, Bwana, utufungulie. Akajibu akasema, Amin, nawaambia, siwajui ninyi. Basi kesheni, kwa sababu hamwijui siku wala saa.”

 

Chagua Hekima!

Tungeweza kuchambua maswala mengi sana yanayozungumzia upumbavu lakini muda usingelitosha, ni ukweli ulio wazi ya kuwa maandiko yanatuonyesha wazi kuwa upumbavu ni tatizo na janga zito sana kuliko hata dhambi zenyewe, kwani hakuna dhambi ambayo utaifanya na isiwe kuwa hukufanya upumbavu, ziko tabia mbaya nyingi sana ambazo mtu akizitenda kimaandiko anaitwa amefanya upumbavu, swali kubwa la kujiuliza Je wewe nawe utakuwa kama mmoja wa wapumbavu? Kama hutaki neno la Mungu linatushauri kuchagua hekima na hii ndio namna ya kuchagua hekima.

a.       Hekima ya kweli inapatikana kwa kumcha Mungu – Mithali 1:7 “Kumcha Bwana ni chanzo cha maarifa, Bali wapumbavu hudharau hekima na adabu”.

 

b.      Uko umuhimu wa kumuomba Mungu hekima – Yakobo 1:5-6    Lakini mtu wa kwenu akipungukiwa na hekima, na aombe dua kwa Mungu, awapaye wote, kwa ukarimu, wala hakemei; naye atapewa.Ila na aombe kwa imani, pasipo shaka yo yote; maana mwenye shaka ni kama wimbi la bahari lililochukuliwa na upepo, na kupeperushwa huku na huku.”

 

2Nyakati 1:7-12 “Usiku ule Mungu akamtokea Sulemani, akamwambia, Omba utakalo nikupe. Sulemani akamwambia Mungu, Umemfanyia baba yangu Daudi fadhili kuu, nawe umenimilikisha mimi badala yake. Basi sasa, Ee Bwana Mungu, na limyakinie baba yangu Daudi neno lako; maana umenitawaza niwe mfalme juu ya watu wengi kama mavumbi ya nchi. Basi sasa nipe hekima na maarifa, nijue kutoka na kuingia mbele ya watu hawa; kwa kuwa ni nani awezaye kuwahukumu watu wako hawa walio wengi? Naye Mungu akamwambia Sulemani, Kwa sababu neno hili lilikuwamo moyoni mwako, wala hukujitakia mali, wala utajiri, wala utukufu, wala maisha za wakuchukiao, wala hukujitakia maisha ya siku nyingi; bali umejitakia hekima na maarifa, upate kuwahukumu watu wangu, niliokutawaza juu yao; basi hekima na maarifa umepewa; nami nitakupa mali, na utajiri, na utukufu, kupita walivyokuwa navyo wafalme wote waliokuwa kabla yako, wala baada yako hapatakuwa na mtu atakayekuwa navyo.”   

 

c.       Hekima ni ulinzi – ukiwa na hekima hakuna kitu kitaharibika kila kitu kitarahisishwa kama vile fedha ilivyo ulinzi hekima itatuhifadhi zaidi kuliko fedha, tutapunguza kuharibikiwa endapo tutachagua hekima, Hekima ni njema hekima ni bora.

 

Muhubiri 7:11-12 “Hekima ni njema, mfano wa urithi; Naam, nayo ni bora kwao walionao jua. Kwa maana hekima ni ulinzi, kama vile fedha ilivyo ulinzi; na ubora wa maarifa ni ya kwamba hekima humhifadhi yeye aliye nayo.”                

 

d.      Chagua Hekima – Mithali 8:4-11 “Enyi watu, nawaita ninyi; Na sauti yangu ni kwa wanadamu.Enyi wajinga, fahamuni werevu, Nanyi wapumbavu, mpate moyo wa kufahamu. Sikieni, maana nitasema yaliyo mazuri, Na kufumbua midomo yangu kutakuwa maadili. Maana kinywa changu kitasema kweli, Na uovu ni chukizo kwa midomo yangu. Maneno yote ya kinywa changu yana haki; Hapana hata neno lililopotoka au la ukaidi. Yote humwelea yule afahamuye, Yote huelekea mbele yao waliopata maarifa.Pokea mafundisho yangu, wala si fedha, Na maarifa kuliko dhahabu safi. Maana hekima ni bora kuliko marijani; Wala vyote vinavyotamanika havilingani nayo.”

Ni muhimu kujikumbusha tena ya kuwa kukosa hekima ni gharama kubwa sana, kwani kinyume cha kukosa hekima ni kuwa mpumbavu, kila unachokiona duniani hakiendi vizuri ni kwa sababu watu walifanya upumbavu, upumbavu ni gharama kubwa sana na umewagharimu wengi, majuto makubwa sana duniani yamechangiwa na upumbavu uliofanywa na watu, sisi kama watu wa Mungu tunapaswa kumuomba Mungu atupe akili, atupe hekima ili tusifanye upumbavu, ambao unaweza kuja kuyagharimu maisha yetu na maisha ya wengine, maandiko yanatutaka tutembee na wenye hekima nasi tutakuwa na hiyo hekima.

Mithali 13:20 “Enenda pamoja na wenye hekima, nawe utakuwa na hekima; Bali rafiki wa wapumbavu ataumia.”

Ni mwenye hekima gani ambaye unaweza kuambatana naye au kwenda naye naye atakuambukiza hekima? Kwa kawaida wenye hekima pia huishi maisha matakatifu na ni nani aliye mtakatifu ni Yesu Kristo ambaye yeye anaitwa Hekima yetu yeye ni mkuu kuliko Suleimani na ana hekima kuliko Sulemani.

1Wakorintho 1:20-24 “Yu wapi mwenye hekima? Yu wapi mwandishi? Yu wapi mlete hoja wa zamani hizi? Je! Mungu hakuifanya hekima ya dunia kuwa ni upumbavu? Kwa maana katika hekima ya Mungu, dunia isipopata kumjua Mungu kwa hekima yake, Mungu alipenda kuwaokoa waaminio kwa upuzi wa lile neno linalohubiriwa. Kwa sababu Wayahudi wanataka ishara, na Wayunani wanatafuta hekima;bali sisi tunamhubiri Kristo, aliyesulibiwa; kwa Wayahudi ni kikwazo, na kwa Wayunani ni upuzi; bali kwao waitwao, Wayahudi kwa Wayunani, ni Kristo, nguvu ya Mungu, na hekima ya Mungu.”

Mathayo 12:41-42 “Watu wa Ninawi watasimama siku ya hukumu pamoja na watu wa kizazi hiki, nao watawahukumu kuwa wamekosa; kwa sababu wao walitubu kwa mahubiri ya Yona; na hapa yupo aliye mkuu kuliko Yona. Malkia wa kusini atasimama siku ya hukumu pamoja na watu wa kizazi hiki, naye atawahukumu kuwa wamekosa; kwa sababu yeye alikuja kutoka pande za mwisho za dunia ili asikie hekima ya Sulemani, na hapa yupo aliye mkuu kuliko Sulemani.”

Kwa kuwa Yesu ndiye hekima yetu natoa ushauri kama maandiko yasemavyo, mpokee Yesu aliye hekima yetu ili kwamba uweze kuishi maisha ya neema na kujifunza kuwa kama yeye na kuishi maisha yasiyo na majuto chagua hekima mchague Yesu.Kumchagua Yesu ni Kuchagua hekima, na kuishi sawa na neno la Mungu ni kufuata njia ya Hekima, Bwana ampe neema kila mmoja wetu kuishi na kuenenda kwa hekima katika jina la Yesu Kristo ameen.  

Rev. Innocent Samuel Kamote.

Mkuu wa wajenzi mwenye hekima.

Jumamosi, 21 Septemba 2024

Kwa nini hatuwezi kunyamaza!


Isaya 62:1-3 “Kwa ajili ya Sayuni sitanyamaza, na kwa ajili ya Yerusalemu sitatulia, hata haki yake itakapotokea kama mwangaza, na wokovu wake kama taa iwakayo. Na mataifa wataiona haki yako, na wafalme wote watauona utukufu wako; nawe utaitwa jina jipya, litakalotajwa na kinywa cha Bwana. Nawe utakuwa taji ya uzuri katika mkono wa Bwana, na kilemba cha kifalme mkononi mwa Mungu wako.”




Utangulizi:

Miaka mingi nyuma Muhubiri na mtumishi wa Mungu Bill Bright aliwahi kuhubiri ujumbe unaofanana na wa kwangu ambao aliuita “Why we cannot remain Silence” kwa tafasiri isiyo rasimi “kwanini hatuwezi kukaa kimya” ujumbe huo umehifadhiwa katika kitabu kiitwacho 50 Great sermon, Yeye alikuwa akizungumzia kuhusu umuhimu wa kuihubiri injili kutokana na Agizo kuu la Bwana wetu Yesu Kristo kwa kanisa na Dr Martin Luther king Jr aliyekuwa mtumishi wa Mungu na mpigania haki za weusi wakati wa ubaguzi  wa rangi kule Marekani aliwahi kusema “Our lives begin to end the day we become silent” pia kwa tafasiri isiyo rasmi ni kama anasema “Maisha yetu huanza kuisha siku tutakapokaa kimya” wote hawa walihubiri na kusema hayo katika mukhtadha tofauti na maandiko tofauti, Bill akizungumzia umuhimu wa agizo kuu hatuwezi kukaa kimya bila kuieneza injili, na Martin akizungumzia kutokuacha kukemea matendo ya  ubaguzi, Hatuwezi kukaa kimya bila kukemea matendo yasiyo ya haki ya kibaguzi,  Leo na mimi nakuja na ujumbe huu kwanini hatuwezi kunyamaza katika mlengo mwingine hasa nikitaka kusisitiza jinsi Roho Mtakatifu anavyofanya kazi ndani yetu ya kutufanya tutimize wajibu, alioweka ndani yetu; kwa hiyo mimi nazungumzia ni nani anayesababisha tusikae kimya, Roho Mtakatifu ambaye amemuita kila mmoja wetu kwa kazi zake maalumu pia anaweka ndani yetu Mzigo “burden” ambao anataka kila mmoja wetu aweze kuutimiza katika maisha yetu hapa Duniani na kwaajili ya hayo utaweza kuona ni vigumu kwetu kuwa na utulivu, bila kutimiza kile ambacho Mungu amekikusudia ndani yetu tutajifunza somo hili kwanini hatuwezi kunyamaza kwa kuzingatia vipengele vitatu vifuatavyo:-


·         Maana ya kunyamaza.

·         Kwanini hatuwezi kunyamaza.

·         Mifano ya kibiblia ya watu walioshindwa kunyamaza.


Maana ya kunyamaza.

Ni muhimu kufahamu kuwa neno kunyamaza halina misamiati mingi katika lugha ya Kiebrania na kiyunani inayoweza kutosheleza kuelezea, Neno kunyamaza au kutulia au kukaa kimya katika kingereza ni neno “Quiet”, ambalo tafasiri yake ni without noise, absence of noise yaani paipo kelele, au bila ya kelele, Lakini  katika lugha ya kiebrania neno linalotumika kuelezea ukimya au utulivu ni neno tām – kwa kiingereza “Gentle” ambalo maana yake ni kutokuchukua hatua, yaani kwa mfano mtu anaweza kutenda kosa ambalo kiimani au kimila ni kosa kubwa sana ambalo linahitaji uchukue hatua kali lakini badala yake unatulia bila kuchukua hatua zozote wala kukemea wala kukosoa wala kusema, au mtu anaweza akawa anakusingizia au kusema maneno ya uzushi na uongo kukuhusu, au akijifanya anathibitisha kuwa wewe una kosa hili au lile kisha wewe hujibu kitu chochote huko kunaitwa kunyamaza  tām kwa kiebrania, kunyamaza kwingineko ni kupuuzia na kut4okuchangia lolote kwa kiyunani linatumika neno “Siōpaō” ambalo maana yake  kwa kiingereza ni “muteness”,  na neno lingine ni neno la Kiibrania “shākat” ambalo maana yake be “undisturbed” yaani kutokuwa na shughuli na mtu, kutokujisumbua na maswala ya watu kuachia kile kitu kiende kama kilivyo; huko ndio kunyamaza kunakotajwa katika maandiko.  Mfano:-

Mwanzo 34:1-7 “Basi Dina, binti Lea, ambaye Lea alimzalia Yakobo, akatoka kuwaona binti za nchi. Shekemu, mwana wa Hamori, Mhivi, mkuu wa nchi, akamwona akamtwaa, akalala naye, akambikiri.Moyo wake ukaambatana na Dina binti Yakobo, akampenda huyu msichana, akasema na huyu msichana kwa maneno mazuri. Shekemu akamwambia Hamori, babaye, akasema, Unipatie msichana huyu awe mke wangu. Basi Yakobo akasikia ya kwamba amembikiri Dina, binti yake. Na wanawe walikuwako pamoja na wanyama wake nyikani. YAKOBO AKANYAMAZA, hata walipokuja. Akatoka Hamori, babaye Shekemu, kumwendea Yakobo, aseme naye.Wanawe Yakobo waliposikia hayo, wakaja kutoka nyikani; nao wakasikitika sana, wakakasirika mno, kwa sababu amefanya upumbavu katika Israeli kwa kulala na binti Yakobo, neno lisilojuzu kutendeka.”

Mwanzo 35:21-22Kisha akasafiri Israeli akapiga hema yake upande wa pili wa mnara wa Ederi. Ikawa Israeli alipokuwa akikaa katika nchi ile, Reubeni akaenda akalala na Bilha, suria wa babaye; ISRAELI AKASIKIA HABARI. Basi hao wana wa Yakobo walikuwa kumi na wawili.”

Mwanzo 25:23-27 “BWANA akamwambia, Mataifa mawili yamo tumboni mwako, Na kabila mbili za watu watafarakana tangu tumboni mwako. Kabila moja litakuwa hodari kuliko la pili, Na mkubwa atamtumikia mdogo. Siku zake za kuzaa zilipotimia, tazama! Mapacha walikuwamo tumboni mwake. Wa kwanza akatoka, naye alikuwa mwekundu mwili wote kama vazi la nywele. Wakamwita jina lake Esau. Baadaye ndugu yake akatoka, na mkono wake unamshika Esau kisigino. Akaitwa jina lake Yakobo. Isaka alikuwa mwenye miaka sitini mkewe alipowazaa. Watoto wakakua, Esau alikuwa mtu ajuaye kuwinda wanyama, mtu wa nyikani, na YAKOBO ALIKUWA MTU MTULIVU, mwenye kukaa hemani.”

Mathayo 26:59-63 “Basi wakuu wa makuhani na baraza yote wakatafuta ushuhuda wa uongo juu ya Yesu, wapate kumwua;wasiuone wangawa walitokea mashahidi wa uongo wengi. Hata baadaye wawili wakatokea, wakasema, Huyu alisema, Naweza kulivunja hekalu la Mungu, na kulijenga kwa siku tatu. Kisha Kuhani Mkuu akasimama akamwambia, Hujibu neno? Hawa wanakushuhudia nini? Lakini, YESU AKANYAMAZA. Kuhani Mkuu akamwambia, Nakuapisha kwa Mungu aliye hai, utuambie kama wewe ndiwe Kristo, Mwana wa Mungu.”

Marko 14:55-61 “Basi wakuu wa makuhani na baraza yote wakatafuta ushuhuda juu ya Yesu wapate kumwua; wasione. Kwa maana wengi walimshuhudia uongo, walakini ushuhuda wao haukupatana. Hata wengine wakasimama, wakamshuhudia uongo, wakisema, Sisi tulimsikia akisema, Mimi nitalivunja hekalu hili lililofanyika kwa mikono, na katika siku tatu nitajenga jingine lisilofanyika kwa mikono. Wala hata hivi ushuhuda wao haukupatana. Kisha Kuhani Mkuu akasimama katikati, akamwuliza Yesu, akisema, Hujibu neno? Hawa wanakushuhudia nini? LAKINI AKANYAMAZA, WALA HAKUJIBU NENO. Kuhani Mkuu akamwuliza tena, akamwambia, Wewe ndiwe Kristo, Mwana wake Mtukufu?

Waamuzi 18:7 “Ndipo hao watu watano wakaenda zao, wakafika Laisha, wakawaona wale watu waliokuwamo ndani yake, jinsi walivyokaa salama salimini kwa mfano wa walivyokaa hao Wasidoni, wenye starehe na hifadhi, kwa maana hapakuwa na mtu katika nchi hiyo aliyekuwa na amri, aliyeweza kuwatweza katika neno lo lote, nao walikuwa wa mbali na hao Wasidoni, wala hawakuwa na shughuli na mtu ye yote.”                                

Katika vifungu vya maandiko hapo juu tunaona sasa matumizi na neno kunyamaza. Linavyotumika kwa Yakobo linatumika neno “tām” gentle hii inamaanisha kuwa Yakobo au Israel alikuwa ni mkimya au mtulivu kwa kuzaliwa kwa hiyo kukaa kimya ilikuwa ni tabia yake ambayo kimsingi watoto wake Simoni na Lawi hawakuwahi kukubaliana nayo, waliona ni ukimya unaopelekea hata kuonewa. Binti yake alipobakwa Yakobo alikaa kimya, nahata Reuben alipolala na suria wa baba yake Yakobo alisikia lakini alikaa kimya, kwa hiyo ni wazi kuwa alikuwa ni mtulivu mno upole uliokithiri, utulivu uliopittiliza, alikaa kimya.

Na kwa Bwana Yesu ukimya wake wakati akiwa anashitakiwa mashitaka ya uongo mbele ya mahakama ya kiyahudi yeye alinyamaza “Siōpaō” muteness Ukimya huu ni ukimya wa kupuuzia, au kuamua kupuuzia na kutokutilia maanani maswala ya kipuuzi. Usipoteze muda wako kujibu lolote unalozushiwa ambalo ni la uongo, Yesu watu walipomsingizia na kusema uongo hakujibu lolote alitulia kimya

Na ukimya unaozungumzwa katika andiko kutoka katika kitabu cha waamuzi linazunguiza utulivu wa kukaa kwa amani au bila kusumbuana na maswala ya watu “shākat” yaani “undisturbed” husumbuliwi wala husumbui, hushughuliki na jambo lolote la mtu wala wao hawashughuliki na wewe kwa hiyo unakaa salama kimyaa

Na neno lingine linalotumika katika maandiko ambalo kisingi ndilo tutakalolitumia leo ni neno la kiibrania “Chshh” ambalo maana yake to keep quiet, to hold peace, au to keep silence   Hili ndio linalotumiwa na Roho Mtakatifu kutokumfanya mtu atulie au awe na Amani au anyamaze wakati kuna mzigo ambao Mungu ameuweka ndani yake

Isaya 62:1-3 “Kwa ajili ya Sayuni sitanyamaza, na kwa ajili ya Yerusalemu sitatulia, hata haki yake itakapotokea kama mwangaza, na wokovu wake kama taa iwakayo. Na mataifa wataiona haki yako, na wafalme wote watauona utukufu wako; nawe utaitwa jina jipya, litakalotajwa na kinywa cha Bwana. Nawe utakuwa taji ya uzuri katika mkono wa Bwana, na kilemba cha kifalme mkononi mwa Mungu wako.”


Kwa nini hatuwezi kunyamaza

Roho Mtakatifu anapokuwa ndani yetu, moja ya kazi anayoifanya ni kukutaharakisha, kukupeleka katika kutimiza majukumu ambayo Mungu ameyakusudia na kuyaweka ndani yako, kwa hiyo yeye hukufanya wewe na mimi tusiweze kukaa kimya, Ni kazi ya Roho Mtakatifu kuwatia nguvu waamini na kuwasukuma moyoni kwa kuwanyima Amani, kwa kuwakoseha utulivu, kwa kuwahimiza na kutowafanya wanyamaze mpaka wametimiza kile ambacho Mungu amekikusudia kwa mtu huyo aweze kukitimiza, kwa hiyo Roho wa Mungu anafanyika “Catalyst” kichocheo  ambaye anainua mioyo yetu na kuweka mzigo na moyo na kutuwezesha kusema kile ambacho Mungu amekikusudia ili kitende kazi ndani yetu mfano kama Mungu anaweka neno ndani yetu basi, Roho Mtakatifu anachochea lile neno ambalo Mungu amelikusudia, tuliseme ili tuweze kulisema na inapotokea utaamua kukaa kimya kunatokea changamoto ndani yako zinazokunyima Amani itakayokupelekea ukaseme kila ambacho Mungu amekikusudia ni kwaajili ya Roho Mtakatifu kuweka kitu ndani yako au ndani yangu ndio tunakosa utulivu au uwezo wa kunyamaza “Chshh” kwanini hatuwezi kunyamaza? Ni kwa sababu Roho Mtakatifu haachi kufanya uchochezi ndani yetu!

Yeremia 1:6-8 “Ndipo niliposema, Aa, Bwana MUNGU! Tazama, siwezi kusema; maana mimi ni mtoto. Lakini Bwana akaniambia, Usiseme, Mimi ni mtoto; maana utakwenda kwa kila mtu nitakayekutuma kwake, nawe utasema kila neno nitakalokuamuru. Usiogope kwa sababu ya hao maana mimi nipo pamoja nawe nikuokoe, asema Bwana.”

Ezekiel 33:7-9 “Basi wewe, mwanadamu, nimekuweka kuwa mlinzi kwa nyumba ya Israeli; basi ulisikie neno hili kinywani mwangu, ukawape maonyo yangu. Nimwambiapo mtu mbaya, Ewe mtu mbaya, hakika utakufa, nawe husemi neno la kumwonya mtu huyo, aiache njia yake, mtu mbaya huyo atakufa katika uovu wake, lakini damu yake nitaitaka mkononi mwako. Walakini ukimwonya mtu mbaya kwa sababu ya njia yake, kusudi aiache; wala yeye asiiache; atakufa huyo katika uovu wake, lakini wewe umejiokoa roho yako.”

Kwa hiyo kumbe Mungu anapoweka neno lake au wajibu wake kwa mtumishi Fulani wa Mungu, Roho Mtakatifu huchochea na kumfanya mtu huyo kukosa utulivu mpaka atakapotimiza kile ambacho Mungu amekiweka, matukio ya aina hii yanaweza kuwekwa kwa waombaji, yanaweza kuwekwa kwa wajumbe wa kinabii ambao Mungu anataka wapeleke maonyo na kutia moyo, wajumbe wa kiinjilisti ambao Mungu anawataka waseme habari njema, wajumbe wa kialimu ambao Mungu anawataka wafundishe, wajumbe wa kiandishi ambao Mungu anawataka waandike “haya uyaonayo uyaandike!” , Wajumbe wa kichungaji ambao Mungu anaweka mzigo ndani yao wachunge na kulisha kundi la kondoo wa Bwana, wajumbe wa kitume ambao watapanda makanisa na kuipeleka injili kule Mungu anakotaka, Wajumbe wa kitaaluma ambao Mungu anataka wawake na kupanda taaluma katika jamii, wakati wote Mungu Roho Mtakatifu atawataharakisha watu wake wasikae kimya kwaajili ya kazi zote katika ufalme wa Mungu, yeye huhimiza na kutoa maelekezo kwa kila muhusika kwaajili ya kazi husika ambayo yeye anataka itimizwe

Ezra 5:1-2 “Basi manabii, Hagai nabii, na Zekaria mwana wa Ido, wakawafanyia unabii Wayahudi waliokuwako Yerusalemu na Yuda; waliwafanyia unabii kwa jina la Mungu wa Israeli. Ndipo akaondoka Zerubabeli, mwana wa Shealtieli, na Yoshua, mwana wa Yosadaki, wakaanza kuijenga nyumba ya Mungu iliyoko Yerusalemu; na pamoja nao walikuwa manabii wa Mungu, wakiwasaidia.”

Matendo 8:26-29 “Malaika wa Bwana akasema na Filipo, akamwambia, Ondoka ukaende upande wa kusini hata njia ile itelemkayo kutoka Yerusalemu kwenda Gaza; nayo ni jangwa. Naye akaondoka, akaenda; mara akamwona mtu wa Kushi, towashi, mwenye mamlaka chini ya Kandake malkia wa Kushi, aliyewekwa juu ya hazina yake yote; naye alikuwa amekwenda Yerusalemu kuabudu, akawa akirejea, ameketi garini mwake akisoma chuo cha nabii Isaya. Roho akamwambia Filipo, Sogea karibu na gari hili, ukashikamane nalo.”

Luka 2:25-35 “Na tazama, pale Yerusalemu palikuwa na mtu, jina lake Simeoni, naye ni mtu mwenye haki, mcha Mungu, akiitarajia faraja ya Israeli; na Roho Mtakatifu alikuwa juu yake.Naye alikuwa ameonywa na Roho Mtakatifu ya kwamba hataona mauti kabla ya kumwona Kristo wa Bwana. Basi akaja hekaluni ameongozwa na Roho; na wale wazazi walipomleta mtoto Yesu ndani, ili wamfanyie kama ilivyokuwa desturi ya sheria, yeye mwenyewe alimpokea mikononi mwake, akamshukuru Mungu, akisema,Sasa, Bwana, wamruhusu mtumishi wako, Kwa amani, kama ulivyosema; Kwa kuwa macho yangu yameuona wokovu wako,Uliouweka tayari machoni pa watu wote; Nuru ya kuwa mwangaza wa Mataifa, Na kuwa utukufu wa watu wako Israeli. Na babaye na mamaye walikuwa wakiyastaajabia hayo yaliyonenwa juu yake. Simeoni akawabariki, akamwambia Mariamu mama yake, Tazama, huyu amewekwa kwa kuanguka na kuinuka wengi walio katika Israeli, na kuwa ishara itakayonenewa. Nawe mwenyewe, upanga utaingia moyoni mwako, ili yafunuliwe mawazo ya mioyo mingi   

2Petro 1:20-21 “Mkijua neno hili kwanza, ya kwamba hakuna unabii katika maandiko upatao kufasiriwa kama apendavyo mtu fulani tu. Maana unabii haukuletwa po pote kwa mapenzi ya mwanadamu; bali wanadamu walinena yaliyotoka kwa Mungu, wakiongozwa na Roho Mtakatifu.”                       

Wakati wote Roho Mtakatifu aliwapa uchochezi manabii, mitume na watumishi mbalimbali wa Mungu kuweza kutoa ujumbe, kutabiri na kutia moyo au kuongoza katika haki ili mapenzi ya Mungu yaweze kufahamika na kutendeka katika jamii ya watu ambao Mungu aliwakusudia, Mungu Roho Mtakatifu anapokuwa amekusudia hilo na wewe ndie ambaye umekusudiwa upeleke ujumbe huo basi yeye hatakuacha unyamaze atakusukuma kwa jambo hilo, utaona moto ndani yako, utaona msukumo, utaona kukosa Amani, utaona kusumbuliwa utasikia kushikwa, kukamatwa, kupelekwa kutaharakishwa kuuzishwa mpaka umetenda kile ambacho kimekusudiwa naye


Mifano ya kibiblia ya watu walioshindwa kunyamaza.

Waamuzi 13:24-25 “Basi yule mwanamke akamzaa mtoto mwanamume akamwita jina lake Samsoni, mtoto huyu akakua, Bwana akambarikia. Roho ya Bwana ikaanza kumtaharakisha katika Mahane-dani, katikati ya Sora na Eshtaoli.”

Wote tunafahamu kuwa Samsoni alizaliwa kwa kusudi maalumu, na Mungu alikuwa amemuandaa kuwa mwokozi wa wana wa Israel ambao walikuwa wanaonewa na Wafilisti kwa wakati huo, tunasoma tu kuwa mara baada ya mtoto huyu kukua Roho ya Bwana ikaanza kumtaharakisha maana yake ikamnyima kutulia, ikamnyima kunyamaza Roho Mtakatifu alianza kuweka msukumo na kumfanya ajione hawezi kutulia ni lazima aseme alijiona hawezi kuwa utumwani yeye wala ndugu zake alijisikia kuwa ni lazima afanye kazi yake aliyopewa ya kuwaokoa wana wa Israel kama Jeshi la Mtu mmoja na alikuwa na hisia zilizokuwa zikimuelekeza au kumyima Amani mpaka atafute kisa ili mradi aweze kuwaokoa wana wa Israel, kwa hiyo tunajifunza hapa kuwa Mungu akikupa agizo huwezi kutulia kunakuwepo moto unaokutesa na kukusumbua ukikutaka utimize kusudi ambalo kwa sababu ya hilo ulizaliwa.       

Isaya 58:1-14 “Piga kelele, usiache, Paza sauti yako kama tarumbeta; Uwahubiri watu wangu kosa lao, Na nyumba ya Yakobo dhambi zao. Walakini wanitafuta kila siku; hupenda kujua njia zangu; kama vile taifa waliotenda haki, wasioacha sheria ya Mungu wao, hutaka kwangu amri za haki; hufurahi kumkaribia Mungu. Husema, Mbona tumefunga, lakini huoni? Mbona tumejitaabisha nafsi zetu, lakini huangalii? Fahamuni, siku ya kufunga kwenu mnatafuta anasa zenu wenyewe, na kuwalemea wote watendao kazi kwenu.

Tazama, ninyi mwafunga mpate kushindana na kugombana, na kupiga kwa ngumi ya uovu. Hamfungi siku hii ya leo hata kuisikizisha sauti yenu juu.  Je! Kufunga namna hii ni saumu niliyoichagua mimi? Je! Ni siku ya mtu kujitaabisha nafsi yake? Ni kuinama kichwa kama unyasi, na kutanda nguo za magunia na majivu chini yake? Je! Utasema ni siku ya kufunga, na ya kukubaliwa na Bwana?  Je! Saumu niliyoichagua, siyo ya namna hii? Kufungua vifungo vya uovu, kuzilegeza kamba za nira, kuwaacha huru walioonewa, na kwamba mvunje kila nira?  Je! Siyo kuwagawia wenye njaa chakula chako, na kuwaleta maskini waliotupwa nje nyumbani kwako? Umwonapo mtu aliye uchi, umvike nguo; wala usijifiche na mtu mwenye damu moja nawe? Ndipo nuru yako itakapopambazuka kama asubuhi, na afya yako itatokea mara; na haki yako itakutangulia; utukufu wa Bwana utakufuata nyuma ukulinde. Ndipo utaita, na Bwana ataitika; utalia, naye atasema, Mimi hapa. Kama ukiiondoa nira; isiwepo kati yako, wala kunyosha kidole, wala kunena maovu; na kama ukimkunjulia mtu mwenye njaa nafsi yako, na kuishibisha nafsi iliyoteswa; ndipo nuru yako itakapopambazuka gizani; na kiwi chako kitakuwa kama adhuhuri. Naye Bwana atakuongoza daima, ataishibisha nafsi yako mahali pasipokuwa na maji, na kuitia nguvu mifupa yako; nawe utakuwa kama bustani iliyotiwa maji, na kama chemchemi ambayo maji yake hayapungui.

Na watu wako watapajenga mahali palipokuwa ukiwa; utaiinua misingi ya vizazi vingi; nawe utaitwa, Mwenye kutengeneza mahali palipobomoka; na, Mwenye kurejeza njia za kukalia. Kama ukigeuza mguu wako usihalifu sabato, usifanye anasa yako siku ya utakatifu wangu; ukiita sabato siku ya furaha, na siku takatifu ya Bwana yenye heshima; ukiitukuza, kwa kutokuzifanya njia zako mwenyewe, wala kuyatafuta yakupendezayo, wala kusema maneno yako mwenyewe; ndipo utakapojifurahisha katika Bwana; nami nitakupandisha mahali pa nchi palipoinuka; nitakulisha urithi wa Yakobo baba yako; kwa maana kinywa cha Bwana kimenena hayo.”               

Nabii Isaya aliitwa na Mungu na Mungu alimtaka awaonye wana wa Israel na kuwaeleza kosa lao ili yamkini waweze kutubu, ujumbe wa makemeo wakati mwingine sio ujumbe mwepesi, kama mwanadamu wakati mwingine alisita na au aliingia hofu  na labda alitaka kuacha lakini Roho wa Mungu alimwambia piga kelele wala usiache paza sauti yako kama tarumbeta kwa nguvu onya juu ya unafiki, wa watu wa Mungu, wakati mwingine ni ngumu kuhubiri maneno magumu watu wanaweza kusema ya kuwa unawahukumu na hasa na wewe ukijijua kuwa u mwanadamu hivyo ilikuwa ni sahihi kwa Isaya kusita sita Lakini aliambiwa apige kelele kama tarumbeta awaonye watu, alipaswa kuwa muaminifu kuhubiri ujumbe wote wa Mungu kama ni toba anyooshe, kama ni rehema anyoooshe na asiseme tu maneno laini kama watu walivyokuwa wanataka kwaajili ya hayo Isaya hakunyamaza.

Isaya 58:1 “Piga kelele, usiache, Paza sauti yako kama tarumbeta; Uwahubiri watu wangu kosa lao, Na nyumba ya Yakobo dhambi zao.”

Wakati wote kumbe Roho wa Mungu anapokuwa juu yako kwaajili ya huduma ambayo Mungu ameiweka ndani yako ni ukweli ulio wazi hutatulia, wala hutanyamaza utafanya kile ambacho Mungu amekikusudia, kama ni kuwafungua watu, kama ni kuponya kama ni kujenga mioyo ya watu, kama ni kutangaza habari njema, yeye hatakuacha utulie atataka utangaze kile ambacho Mungu anataka kukifanywa kupitia wewe ilikuwa hivyo kwa Isaya nabii na ilikuwa hivyo kwa Masihi Bwana wetu Yesu.

Isaya 61:1-3 “Roho ya Bwana MUNGU i juu yangu; kwa sababu Bwana amenitia mafuta niwahubiri wanyenyekevu habari njema; amenituma ili kuwaganga waliovunjika moyo, kuwatangazia mateka uhuru wao, na hao waliofungwa habari za kufunguliwa kwao.Kutangaza mwaka wa Bwana uliokubaliwa, na siku ya kisasi cha Mungu wetu; kuwafariji wote waliao; kuwaagizia hao waliao katika Sayuni, wapewe taji ya maua badala ya majivu, mafuta ya furaha badala ya maombolezo, vazi la sifa badala ya roho nzito; wapate kuitwa miti ya haki, iliyopandwa na Bwana, ili atukuzwe.”

Ni maneno ya Nabii Isaya lakini vilevile ni ya Masihi, Yesu alipokuja duniani aliyatumia maneno haya, ni kazi ileile ya Roho Mtakatifu ambaye hataki  mtu mwenye agizo kunyamaza, Roho wa Mungu kupitia Yesu alitaka afungue kinywa chake na kuwahubiria wanyenyekevu habari njema, alitakiwa kuwaganga waliovunjika moyo, alitakiwa kutangaza uhuru kwa mateka, na wafungwa kuwatangazia kufunguliwa, na kuutangaza mwaka wa neema uliokubalika, wasingeliweza kunyamaza kimya katika hayo, na ndio maana tunamuona Yesu akizunguka toka mji mmoja kwenda mji mwingine na vijijini kila mahali akiifanya kazi hii asingeliweza kutulia kwa sababu Roho Mtakatifu alimpaka mafuta kwaajili ya hilo, kila mmoja kwa kusudi lake ambalo kwalo Mungu amekupaka mafuta lifanye kwa bidii na kwa uaminifu wote  na kwa usikivu mkubwa kwa Roho wa Mungu na utaona kuwa huna sababu za kunyamaza!

Isaya 62:1-3 “Kwa ajili ya Sayuni sitanyamaza, na kwa ajili ya Yerusalemu sitatulia, hata haki yake itakapotokea kama mwangaza, na wokovu wake kama taa iwakayo. Na mataifa wataiona haki yako, na wafalme wote watauona utukufu wako; nawe utaitwa jina jipya, litakalotajwa na kinywa cha Bwana. Nawe utakuwa taji ya uzuri katika mkono wa Bwana, na kilemba cha kifalme mkononi mwa Mungu wako.”

Isaya anazungumza kwa niaba ya mji wa Yerusalem yaani Sayuni akimaanisha Israel, kwamba pamoja na kukumbwa na matukio mbalimbali na kubomolewa na maadui lakini haitakuja itokee, mji huu usisimame, ni mji ambao uko kwenye mapenzi ya Mungu, ni mji uliowekewa waombezi, manabii, na waombolezaji maarufu, ambao wanauombea usiku na mchana ili kwamba ufalme wa Mungu uweze kusimama, Kama Mungu alivyomuinua Isaya bado anaendelea kuinua watu wanaoiombea Israel kila iitwapo leo katika kila kona za Dunia, wanaoitakia mema Israel wako kama jeshi, Yerusalem ni mji ambao Utawala halisi wa kimasihi utatawala na Kristo akiwa Mfalme wa utawala huo Wakristo wanapoomba katika sala ya Bwana ufalme wako uje na mapenzi ya Mungu yatimizwe hapa duniani kama mbinguni Mathayo 6:10 maana yake tunaomba pia kwamba Yesu arudi na kusimamisha utawala wake hapa duniani na ufalme huo na kiti chake cha Enzi kitakuwa Israel,Pale Yerusalem, Sayuni, Kwaajili ya Israel Hatuwezi kunyamaza

Yeremia 20:7-9 “Ee Bwana, umenihadaa, nami nimehadaika; wewe una nguvu kuliko mimi, ukashinda; nimekuwa kitu cha kuchekesha, mchana kutwa; kila mtu hunidhihaki.Maana kila ninenapo napiga kelele, nalia, Dhuluma na uharibifu! Kwa kuwa neno la Bwana limefanywa shutumu kwangu, na dhihaka, mchana kutwa. Nami nikisema, Sitamtaja, wala sitasema tena kwa jina lake; basi, ndipo moyoni mwangu kumekuwamo kama moto uwakao, uliofungwa ndani ya mifupa yangu, nami nimechoka kwa kustahimili, wala siwezi kujizuia.”             

Yeremia alitumwa na Mungu kumbuka kuwa Mungu aliweka maneno ndani yake na kumuamuru kuyasema haikuwa kitu rahisi kukubalika katika mioyo ya watu kiasi ambacho hata pamoja na kuwa Mungu alimwambia nitakuwa pamoja naye alikutana na magumu sana alitiwa gerezani, aliteswa alitupwa katika shimo  la matope ilifikia hatua alitaka kukaa kimya asiseme lakini kwa kadiri alivyokuwa akijitahidi akae kimya kuna nguvu ya kiungu iliyokuwa inamlazimisha kusema wivu wa kiungu ulijaa ndani yake na alipoona uovu uliokuwa ukiendelea na ujumbe aliopewa kusema maneno yalimuunguza akawa hawezi kuyafumbia mdomo alilazimika kutangaza kile ambacho Mungu alikuwa amemuagiza pamoja na kuwa ilimgharimu mateso makali na maumivu makubwa.

Yeremia 47:6-7 “Ee upanga wa Bwana, Siku ngapi zitapita kabla hujatulia? Ujitie katika ala yako; Pumzika, utulie.Utawezaje kutulia, Ikiwa Bwana amekupa agizo? Juu ya Ashkeloni na juu ya pwani, Ndipo alipoyaamuru hayo.”

Wafilisti walikuwa wanaikalia pwani ya Yuda na mara nyingi kihistoria kulikuwa na ugomvi kati ya nchi ya Israel na wafilisti,  Yeremia alitakiwa kutoa unabii wa kuwaonya wafilisti ya kuwa upanga wa Bwana utawahusu, ni kama Mungu alikuwa ameamuru hukumu kwa wafilisti kuwa upanga wa Bwana uipige Gaza na Ashkeloni, ilionekana kuwa hakutakuwa na utulivu kwa wafilisti, kila wakati Gaza itapigwa, hatujui kama nabii aliwaombea wafilisti angalau upanga utulie Lakini lilikuwa ni agizo la Mungu upanga ulikataa kutulia kwa sababu ulikuwa na agizo la Mungu, utawezaje kutulia ikiwa Bwana amekupa agizo? Kupigwa kwa Gaza ni agizo la kimaandiko na itaendelea kuwa hivyo kwa sababu ndivyo neno la Mungu linavyosema na Roho wa Mungu husukuma hukumu juu ya Gaza kwa sababu ni agizo lililoko katika neno lake.

Yoel 2:28-29 “Hata itakuwa, baada ya hayo, ya kwamba nitamimina roho yangu juu ya wote wenye mwili; na wana wenu, waume kwa wake, watatabiri, wazee wenu wataota ndoto, na vijana wenu wataona maono; tena juu ya watumishi wenu, wanaume kwa wanawake, katika siku zile, nitamimina roho yangu.”

Ni unabii wa maana sana kimsingi unahusiana na siku za mwisho na ujio wa Roho Mtakatifu kama alivyoona Yoel Roho Mtakatifu atakuja na kazi maalumu kwa kila watu na makundi na kila mmoja hataweza kukaaa kimya atasema tu, watatabiri, wanaona maono, wataota ndoto, kwa hiyo tunaweza kukubaliana wote ya kuwa ubatizo wa Roho Mtakatifu utasababisha na kumfanya kila mwanadamu kutokutulia, neno la Mungu linasema tena juu ya watumishi wangu, nini maana yake watumishi maana yake “Bond Servants” ni neno limetumika mara 800 katika maandiko likimaanisha ni watu wa kazi watumwa hawatatulia, kila atakayepewa Roho wa Mungu hataweza kuwa na utulivu atafanya kile ambacho Mungu ambaye ni bwana wetu amekusudia akifanye.  

Mika 3:8 “Bali mimi, hakika nimejaa nguvu kwa roho ya Bwana; nimejaa hukumu na uwezo; nimhubiri Yakobo kosa lake, na Israeli dhambi yake.”

Mika aliitwa kuwa msemaji kwa niaba ya Mungu yaani nabii, alinena kwa uweza wa Roho Mtakatifu, alitakiwa kuikemea dhambi katika nyumba ya Mungu na ilikuwa ni kazi aliyopewa pamoja na kuonyesha moyo wa Mungu, kutia moyo na kukatisha tamaa uovu, wakati wa Mika kulikuwa na manabii wa uongo wengi, waliokuwa wakiwakosesha watu wa Mungu kwa jumbe zisizo za kweli, lakini uweza wa Roho wa Bwana haukumpa Amani Mika alipewa kusema, alipewa kuonya, alipewa kutangaza hukumu, alipewa kutangaza rehema asingeliweza kunyamaza

Mika 3:5 “Bwana asema hivi katika habari za manabii wanaowakosesha watu wangu; hao waumao kwa meno yao, na kulia, Amani; na mtu awaye yote asiyetia kitu vinywani mwao, wao humwandalia vita.”

Mungu alimtaka Mika kukemea na kusema kweli, bila kujali kuwa liko kundi la manabii feki yaani wa uongo, Kanisa halipaswi kufuata shinikizo la watu Fulani ndani au nje ya nchi wanaotaka tuwe na mtindo Fulani unaofanana wa maisha hata kama mambo hayo ni uovu yako kinyume na Mungu na mila zetu, Kanisa ni lazima likemee bila huruma kile ambacho kinaonekana kuwa ni uongo na kuwa kiko kinyume na mapenzi ya Mungu, Mika hakufuata mkumbo alibaki katika zamu yake na kukemea kweli kweli kwa sababu nyuma yake kulikuwa na shinikizo la Roho Mtakatifu kwanini hatuwezi kunyamaza kwa sababu Roho wa Mungu anafanya hivyo ndani yetu, hakuna anayeweza kutulia!

Zekaria 4:6-9 “Akajibu akaniambia, akisema, Hili ndilo neno la Bwana kwa Zerubabeli, kusema, Si kwa uwezo, wala si kwa nguvu, bali ni kwa roho yangu, asema Bwana wa majeshi.Nani wewe, Ee mlima mkubwa? Mbele ya Zerubabeli utakuwa nchi tambarare; naye atalileta lile jiwe la kuwekwa juu kabisa pamoja na vigelegele vya, Neema, neema, ilikalie. Tena neno la Bwana likanijia, kusema, Mikono yake Zerubabeli imeiweka misingi ya nyumba hii, na mikono yake ndiyo itakayoimaliza; nawe utajua ya kuwa Bwana wa majeshi amenituma kwenu.”

Mungu alimuinua Zerubabeli kuijenga tena Nyumba ya Mungu katika mazingira magumu wakati Israel waliporejea kutoka utumwani Babeli yaani wayahudi, kazi hii ilikuwa ngumu kiasi ambacho kuna wakati watu walikuwa kama wameisusia, Lakini Mungu aliwainua manabii Habakuki, Zekaria na Malaki kuwatia moyo viongozi waliokuwa wanahusika na agizo la kuijenga nyumba ya Bwana walipokuwa wanasita sita Zekaria alipewa ujumbe kumtia Moyo Zerubabeli kuwa nyumba hiyo itajengeka tu sio kwa uweza wa kiserikali wala wa kijeshi bali Roho Mtakatifu, huyu atainua hari ya wajenzi na watajenga kwa uwezo wake hakuna mtu atakayeweza kutulia kwa sababu Roho wa Mungu atasababisha kazi yake itendeke na hakuna kikwazo chochote kitakachoweza kusimama mbele ya wajenzi.

Matendo 1:8 “Lakini mtapokea nguvu, akiisha kuwajilia juu yenu Roho Mtakatifu; nanyi mtakuwa mashahidi wangu katika Yerusalemu, na katika Uyahudi wote, na Samaria, na hata mwisho wa nchi.”    

Ni tangazo la ujio wa Roho Mtakatifu kwa kanisa, mitume waliagizwa kusubiria ubatizo huo na walihakikishiwa kuwa watakapopokea ubatizo wa Roho Mtakatifu hawataweza kukaa kimya watasema, watahubiri, watathibitisha na kuwa wao ni mashahidi wa kweli kwaajili ya Yesu kristo, hatakuja kuwa na kizuizi watamtii Mungu kuliko wanadamu katika swala zima la kuhubiri injili.

Matendo 5:17-32 “Akaondoka Kuhani Mkuu na wote waliokuwa pamoja naye, (hao ndio walio wa madhehebu ya Masadukayo), wamejaa wivu, wakawakamata mitume wakawaweka ndani ya gereza; lakini malaika wa Bwana akafungua milango ya gereza usiku, akawatoa, akasema, Enendeni mkasimame hekaluni mkawaambie watu maneno yote ya Uzima huu. Nao waliposikia wakaenda alfajiri hekaluni, wakaanza kufundisha. Akaja Kuhani Mkuu nao waliokuwa pamoja naye, wakawakutanisha watu wa baraza, na wazee wote wa wana wa Israeli, wakatuma watu gerezani ili wawalete. Hata watumishi walipofika hawakuwaona gerezani, wakarudi wakatoa habari, wakisema, Gereza tumeikuta imefungwa salama, nao walinzi wamesimama mbele ya mlango; lakini tulipoufungua hatukukuta mtu ndani. Basi jemadari wa hekalu na wakuu wa makuhani waliposikia haya, wakaingiwa na shaka kwa ajili yao, litakuwaje jambo hilo. Mtu mmoja akaja akawapasha habari ya kwamba, Watu wale mliowaweka gerezani wako ndani ya hekalu, wamesimama wakiwafundisha watu. Ndipo yule jemadari akaenda pamoja na watumishi, wakawaleta, lakini si kwa nguvu, kwa maana waliogopa watu wasije wakawapiga kwa mawe. Walipowaleta, wakawaweka katika baraza. Kuhani Mkuu akawauliza, akisema, Je! Hatukuwaamuru ninyi kwa nguvu, msifundishe kwa jina hili? Nanyi, tazameni, mmeijaza Yerusalemu mafundisho yenu, na mnataka kuileta damu ya mtu yule juu yetu. Petro na mitume wakajibu, wakisema, Imetupasa kumtii Mungu kuliko wanadamu. Mungu wa baba zetu alimfufua Yesu, ambaye ninyi mlimwua mkimtundika katika mti. Mtu huyo Mungu amemtukuza kwa mkono wake wa kuume, awe Mkuu na Mwokozi, awape Waisraeli toba na msamaha wa dhambi. Na sisi tu mashahidi wa mambo haya, pamoja na Roho Mtakatifu ambaye Mungu amewapa wote wamtiio.”

Mitume walikuwa na agizo la kuihubiri injili, na Mungu Roho Mtakatifu alikuwa amewabatiza kusudi waweze kulitimiza kusudi hilo pana la Mungu, hata hivyo walikutana na upinzani mkali kutoka kwa wazee wa kiyahudi wajulikanao kama Sanhedrin yaani mahakama kuu ya kiyahudi, hawa waliwakataza wasihurbiri wala wasiseme kitu kuhusu Yesu, waliwatia gerezani lakini hata hivyo malaika wa Bwana aliwafungulia hawawezi kunyamaza waliagizwa waendelee kufundisha na walifanya hivyo, wazee walikasirika sana  wakiwataka wakae kimyaa Petro  na mitume wakajibu hoja kuwa imetupasaa kumtii Mungu kuliko wanadamu, Roho Mtakatifu hutuwezesha kuwa na utii wa kiwango cha juu kwaajili ya kile ambacho tumeitiwa kukifanya na kufundisha na kulisema neno lake tunawezaje kunyamaza? Kanisa ndio maana hatuwezi kunyamaza na ndio maana hata mimi na wewe hatuwezi kunyamaza.    

Matendo 17:16 “Paulo alipokuwa akiwangojea huko Athene na kuona jinsi mji ule ulivyojaa sanamu, roho yake ilichukizwa sana ndani yake.”

Paulo mtume aliihubiri injili huko Thesalonike na Beroya, hata hivyo wayahudi wenye wivu walimuwinda na kutaka kumua, kwa hiyo wanafunzi waliookoka walimpeleka Paulo katika mji wa Athene ili awasubiri Timotheo na Sillas ambao walibaki katika miji ya awali, Neno la Mungu linatuambia  wakati alipokuwa akiwasubiri huko Athene aliona mji ule umejaa sanamu, roho yake ilichukizwa sana Katika kiingereza tunaambiwa hivi “his spirit was stirred in him” neno stirred katika kiyunani ni “Paroxunō” maana yake easily Provoked  yaani alichochewa, alipatwa na hasira ya kiungu au alisukumwa kutokukaa kimya, Roho Mtakatifu ndani ya Paulo mtume alipoona sanamu hakusubiri aliona itachelewesha akaanza kuhubiri, Roho wa Mungu hatakuacha unyamaze akiwa ameweka kitu au mzigo au wajibu ambao unatakiwa uutekeleze. Je wewe roho yako inachukizwa? Unapoona wanadamu wanaoana na mbwa? unachukizwa na kuona mwanaume akimpa binti yake mimba?, wanadamu wakilala na wanyama, madaktari wakifanya ngono na wagonjwa, watumishi wanapozini na washirika, matajiri wakipewa nafasi ya vyeo vikubwa makanisani, washirika wakiibiwa fedha na kutajirisha wahubiri, Wahubiri wakijilimbikizia mali, kampeni za kisiasa zikitapakaa makanisani, watu wakipeana sumu kwaajili ya nafasi za uongozi, watu wakiombewa bila kuongozwa sala ya toba, wanakwaya wakitembea wenyewe kwa wenyewe, wanamuziki wakiacha waume zao na ndoa zao kwa kisingizio cha wito, unanyamazaje wakati utoaji wa mimba umeingia makanisani hata wanandoa waliookoka siku hizi wanatoa mimba?, madawa ya kuleywa yakiuzwa kila mahali, rushwa na ushoga umetapakaa kila mahali, unanyamazaje wakati watu wakiwa wahanga wa picha za ngono? Uamsho ukisisitizwa bila utakatifu, mafundisho potofu yakiwa hayakemewi, watu wakiwa wanatekwa na kuuawa, mauaji ya kutisha yakisambaa, ulawiti na ubakaji uliokithiri, hali ya uchumi ikiendelea kuwa mbaya? Paulo mtume angekuwepo leo asingeliweza kunyamaza, ikiwa sanamu tu zilimsumbua sana sisi nasi hatunabudi kuhakikisha kuwa tunaifikia jamii na kuijenga kwa gharama yoyote ile na kamwe hatuwezi kunyamaza!, Roho Mtakatifu akiwa ndani yetu roho zetu zitachukizwa hatuwezi kunyamaza!

Warumi 1:16-17 “Kwa maana siionei haya Injili; kwa sababu ni uweza wa Mungu uuletao wokovu, kwa kila aaminiye, kwa Myahudi kwanza, na kwa Myunani pia. Kwa maana haki ya Mungu inadhihirishwa ndani yake, toka imani hata imani; kama ilivyoandikwa, Mwenye haki ataishi kwa imani.”                

Paulo mtume anaonyesha wazi kuwa haionei haya injili kwa sababu ni uweza wa Mungu uletao wokovu kwa watu waaminio, kutokana na uwezo mkubwa wa habari njema kuwasaidia wanadamu na kuwapa uzima wa milele bure kwa Imani katika Kristo Yesu Paulo anaona ana wajibu wa kutokuionea haya injili iwe ni kwa kufungwa au kudhaliliswa, au kuteswa kwa sababu zozote zile hawezi kuona aibu kwa sababu ya injili, maana yake pia hawezi kukaa kimya kwaajili ya injili ataendelea kuisema katika mazingira yoyote.

2Timotheo 1:7-9 “Maana Mungu hakutupa roho ya woga, bali ya nguvu na ya upendo na ya moyo wa kiasi.Basi usiuonee haya ushuhuda wa Bwana wetu, wala usinionee haya mimi mfungwa wake, bali uvumilie mabaya pamoja nami kwa ajili ya Injili, kwa kadiri ya nguvu ya Mungu; ambaye alituokoa akatuita kwa mwito mtakatifu, si kwa kadiri ya matendo yetu sisi, bali kwa kadiri ya makusudi yake yeye na neema yake. Neema hiyo tulipewa katika Kristo Yesu tangu milele,”

Paulo anamkumbusha Timotheo kutokuonea haya ushuhuda wa Bwana, kutokuionea haya ufungwa kwaajili ya injili, anamtaka avumilie mabaya kwaajili ya injili aendelee kwa kadiri ya nguvu za Mungu aliyewaita akimkumbusha kuwa Roho Mtakatifu sio Roho ya woga bali ni ya nguvu na upendo na moyo wa kiasi kwa hiyo haijalishi ni magumu kiasi gani anakutana nayo anamtaka aendelee na kazi ya wito mtakatifu kwa kusudi lile kuu, Roho Mtakatifu huondoa woga wote na kutupa ujasiri, na nguvu na upendo ili tuweze kusonga mbele kwa wito tulioitiwa hivyo hatuwezi kunyamaza, Ni yeye ambaye akiwa ndani yetu tutavurugwa, tutachukizwa na sanamu, tutataharakishwa hatutakubali uonevu wa ibilisi dhidi ya ndugu zetu, tutawaombea watu, tutawafungua watu, tutawapa watu mahitaji yao kwa msukumo wa Roho Mtakatifu ndani yetu ni yeye ni yeye ni yeye anayesababisha hatuwezi kunyamaza kamwe!

2Timotheo 2:8-9 “Mkumbuke Yesu Kristo, aliyefufuka katika wafu, wa uzao wa Daudi kama inenavyo injili yangu. Nami katika hiyo nimeteswa hata kufungwa kama mtenda mabaya; lakini neno la Mungu halifungwi.”

Mwisho Paulo mtume akiwa kifungoni anamkumbusha Timotheo kumkumbuka Yesu aliyefufuka katika wafu, ya kuwa uko ushindi katika maisha yetu ya kazi ya injili kama Daudi alivyoshinda Vita vyote kwa jinsi ya mwili, Yesu naye ameshinda vita vyote vya kiroho, kwa hiyo hata ingawa Paulo mtume alikuwa kifungoni, alimwambia Timotheo kuwa neno la Mungu halifungwi, akiwa kifungoni hakuweza kunyamaza na badala yake alianza kuandika nyaraka zenye kuwatia moyo waamini na watumishi wa Mungu na kuendelea kuwajenga, Katika nyakati zetu leo hata kama tutakuwa gerezani, injili itaendelea kwa sababu Roho Mtakatifu hatatuacha kunyamaza. Neno la Mungu halifungwi! Roho Mtakatifu hatatuacha tuwe na utulivu bila kutimiza ile huduma ya upatanisho aliyoiweka ndani yetu haleluyaa!

Hitimisho

Usinyamaze kwaajili ya kile ambacho Mungu amekuitia kukifanya uwepo wa Roho Mtakatifu katika maisha yetu unatufanya kuwa na msaidizi wa karibu ndani yetu, kiongozi ndani yetu, mwenye kututia nguvu, na anatutia nguvu na kutupa nguvu za ushawishi ndani yetu, Hatuna budi kumtii  na kukubali kuongozwa naye katika kuyatii mapenzi yake na tunapomtii atasema nasi na kutusukuma kama nguvu ya moto ndani yetu akiweka wivu, wa Bwana na kutusukuma katika kuyatii mapenzi yake kwa hiyo ni lazima kuhakikisha kuwa tunaihubiri injili kwa namna yoyote kila mmoja kwa kadiri ya wito wake alioitiwa na kamwe tusiache kwa sababu tukiacha watu watakengeuka, mwenye kuomba asiache kuomba, mwenye kuhubiri asinyamaze, mwenye kutoa asiache, mwenye kuangalia wafungwa asiache, mwenye kufariji wajane na yatima asiache, mwenye kushuhudia asiache, mwenye kufundisha asiache mwenye kusimamia asiache, mwenye kutia moyo asiache na mwenye kuandika kama mimi asiache hakuna anayeweza kutunyamazisha kwa sababu Roho wa Mungu anataka kila kitu kitimizwe ndani yetu kwa wakati wake! 

2Timotheo 4:1-5 “Nakuagiza mbele za Mungu, na mbele za Kristo Yesu, atakayewahukumu walio hai na waliokufa; kwa kufunuliwa kwake na kwa ufalme wake; lihubiri neno, uwe tayari, wakati ukufaao na wakati usiokufaa, karipia, kemea, na kuonya kwa uvumilivu wote na mafundisho. Maana utakuja wakati watakapoyakataa mafundisho yenye uzima; ila kwa kuzifuata nia zao wenyewe watajipatia waalimu makundi makundi, kwa kuwa wana masikio ya utafiti;nao watajiepusha wasisikie yaliyo kweli, na kuzigeukia hadithi za uongo.Bali wewe, uwe na kiasi katika mambo yote, vumilia mabaya, fanya kazi ya mhubiri wa Injili, timiliza huduma yako.”

Warumi 12:4-8 “Kwa kuwa kama vile katika mwili mmoja tuna viungo vingi, wala viungo vyote havitendi kazi moja; Vivyo hivyo na sisi tulio wengi tu mwili mmoja katika Kristo, na viungo, kila mmoja kwa mwenzake. Basi kwa kuwa tuna karama zilizo mbalimbali, kwa kadiri ya neema mliyopewa; ikiwa unabii, tutoe unabii kwa kadiri ya imani; ikiwa huduma, tuwemo katika huduma yetu; mwenye kufundisha, katika kufundisha kwake; mwenye kuonya, katika kuonya kwake; mwenye kukirimu, kwa moyo mweupe; mwenye kusimamia kwa bidii mwenye kurehemu, kwa furaha.”

Roho wa Mungu hututia nguvu katika maisha yetu kuishinda aibu, woga, na vikwazo na kutupa ujasiri na hali ya kutokuweza kukaa kimya akitenda kazi ndani yetu na kututia nguvu na ujasiri na kutuagiza kwa neno lake na kwa sababu hiyo hatuwezi kunyamaza, Martini Luther King Jr alikuwa mchungaji lakini wakati huo ulikuwa ni wakati wa ubaguzi mkubwa wa rangi nchini Marekani, alisimama sio tu kama Muhubiri lakini aliionyesha jamii kuwa matukio ya kibaguzi sio kitu sahihi, hakunyamaza kila lilipojitokeza tukio la kibaguzi na aliuawa kwaajili ya hilo, naamini kuwa Mungu alimtia nguvu, kutokukaa kimya na yeye alisema tutakaa kimya pale tu tutakapokuwa tumekufa, au kwa lugha nyingine Maisha yetu hufikia mwisho pale tu tunapoanza kukaa kimya kwaali ya maswala ya msingi Our lives begin to end the day we become silentBill Bright yeye alisema “Why we cannot remain Silence  kwanini hatuwezi kukaa kimya akikazia kwa sababu tuna agizo kuu la kuihubiri injili, na mimi nimesema kwanini hatuwezi kunyamaza kwa sababu Roho Mtakatifu yuko ndani yetu naye ndiye kichocheo na sababu kwanini hatuwezi kunyamaza.

Wewe nawe kamwe usikae kimya kwa kile ambacho Roho Mtakatifu amekuwekea ndani yako,  Endelea kupiga kelele kama ni za uamsho, kemea kama ni za kukemea manabii wa uongo, kama ni injili ihubiri, unazo sababu lukuki kwanini hauwezi kukaa kimya, tunazo sababu nyingi kwanini hatuwezi kunyamaza haleluyaaa! Uongezewe neema

Rev. Innocent Samuel Kamote

Mkuu wa wajenzi mwenye Hekima