Jumamosi, 21 Septemba 2024

Kwa nini hatuwezi kunyamaza!


Isaya 62:1-3 “Kwa ajili ya Sayuni sitanyamaza, na kwa ajili ya Yerusalemu sitatulia, hata haki yake itakapotokea kama mwangaza, na wokovu wake kama taa iwakayo. Na mataifa wataiona haki yako, na wafalme wote watauona utukufu wako; nawe utaitwa jina jipya, litakalotajwa na kinywa cha Bwana. Nawe utakuwa taji ya uzuri katika mkono wa Bwana, na kilemba cha kifalme mkononi mwa Mungu wako.”




Utangulizi:

Miaka mingi nyuma Muhubiri na mtumishi wa Mungu Bill Bright aliwahi kuhubiri ujumbe unaofanana na wa kwangu ambao aliuita “Why we cannot remain Silence” kwa tafasiri isiyo rasimi “kwanini hatuwezi kukaa kimya” ujumbe huo umehifadhiwa katika kitabu kiitwacho 50 Great sermon, Yeye alikuwa akizungumzia kuhusu umuhimu wa kuihubiri injili kutokana na Agizo kuu la Bwana wetu Yesu Kristo kwa kanisa na Dr Martin Luther king Jr aliyekuwa mtumishi wa Mungu na mpigania haki za weusi wakati wa ubaguzi  wa rangi kule Marekani aliwahi kusema “Our lives begin to end the day we become silent” pia kwa tafasiri isiyo rasmi ni kama anasema “Maisha yetu huanza kuisha siku tutakapokaa kimya” wote hawa walihubiri na kusema hayo katika mukhtadha tofauti na maandiko tofauti, Bill akizungumzia umuhimu wa agizo kuu hatuwezi kukaa kimya bila kuieneza injili, na Martin akizungumzia kutokuacha kukemea matendo ya  ubaguzi, Hatuwezi kukaa kimya bila kukemea matendo yasiyo ya haki ya kibaguzi,  Leo na mimi nakuja na ujumbe huu kwanini hatuwezi kunyamaza katika mlengo mwingine hasa nikitaka kusisitiza jinsi Roho Mtakatifu anavyofanya kazi ndani yetu ya kutufanya tutimize wajibu, alioweka ndani yetu; kwa hiyo mimi nazungumzia ni nani anayesababisha tusikae kimya, Roho Mtakatifu ambaye amemuita kila mmoja wetu kwa kazi zake maalumu pia anaweka ndani yetu Mzigo “burden” ambao anataka kila mmoja wetu aweze kuutimiza katika maisha yetu hapa Duniani na kwaajili ya hayo utaweza kuona ni vigumu kwetu kuwa na utulivu, bila kutimiza kile ambacho Mungu amekikusudia ndani yetu tutajifunza somo hili kwanini hatuwezi kunyamaza kwa kuzingatia vipengele vitatu vifuatavyo:-


·         Maana ya kunyamaza.

·         Kwanini hatuwezi kunyamaza.

·         Mifano ya kibiblia ya watu walioshindwa kunyamaza.


Maana ya kunyamaza.

Ni muhimu kufahamu kuwa neno kunyamaza halina misamiati mingi katika lugha ya Kiebrania na kiyunani inayoweza kutosheleza kuelezea, Neno kunyamaza au kutulia au kukaa kimya katika kingereza ni neno “Quiet”, ambalo tafasiri yake ni without noise, absence of noise yaani paipo kelele, au bila ya kelele, Lakini  katika lugha ya kiebrania neno linalotumika kuelezea ukimya au utulivu ni neno tām – kwa kiingereza “Gentle” ambalo maana yake ni kutokuchukua hatua, yaani kwa mfano mtu anaweza kutenda kosa ambalo kiimani au kimila ni kosa kubwa sana ambalo linahitaji uchukue hatua kali lakini badala yake unatulia bila kuchukua hatua zozote wala kukemea wala kukosoa wala kusema, au mtu anaweza akawa anakusingizia au kusema maneno ya uzushi na uongo kukuhusu, au akijifanya anathibitisha kuwa wewe una kosa hili au lile kisha wewe hujibu kitu chochote huko kunaitwa kunyamaza  tām kwa kiebrania, kunyamaza kwingineko ni kupuuzia na kut4okuchangia lolote kwa kiyunani linatumika neno “Siōpaō” ambalo maana yake  kwa kiingereza ni “muteness”,  na neno lingine ni neno la Kiibrania “shākat” ambalo maana yake be “undisturbed” yaani kutokuwa na shughuli na mtu, kutokujisumbua na maswala ya watu kuachia kile kitu kiende kama kilivyo; huko ndio kunyamaza kunakotajwa katika maandiko.  Mfano:-

Mwanzo 34:1-7 “Basi Dina, binti Lea, ambaye Lea alimzalia Yakobo, akatoka kuwaona binti za nchi. Shekemu, mwana wa Hamori, Mhivi, mkuu wa nchi, akamwona akamtwaa, akalala naye, akambikiri.Moyo wake ukaambatana na Dina binti Yakobo, akampenda huyu msichana, akasema na huyu msichana kwa maneno mazuri. Shekemu akamwambia Hamori, babaye, akasema, Unipatie msichana huyu awe mke wangu. Basi Yakobo akasikia ya kwamba amembikiri Dina, binti yake. Na wanawe walikuwako pamoja na wanyama wake nyikani. YAKOBO AKANYAMAZA, hata walipokuja. Akatoka Hamori, babaye Shekemu, kumwendea Yakobo, aseme naye.Wanawe Yakobo waliposikia hayo, wakaja kutoka nyikani; nao wakasikitika sana, wakakasirika mno, kwa sababu amefanya upumbavu katika Israeli kwa kulala na binti Yakobo, neno lisilojuzu kutendeka.”

Mwanzo 35:21-22Kisha akasafiri Israeli akapiga hema yake upande wa pili wa mnara wa Ederi. Ikawa Israeli alipokuwa akikaa katika nchi ile, Reubeni akaenda akalala na Bilha, suria wa babaye; ISRAELI AKASIKIA HABARI. Basi hao wana wa Yakobo walikuwa kumi na wawili.”

Mwanzo 25:23-27 “BWANA akamwambia, Mataifa mawili yamo tumboni mwako, Na kabila mbili za watu watafarakana tangu tumboni mwako. Kabila moja litakuwa hodari kuliko la pili, Na mkubwa atamtumikia mdogo. Siku zake za kuzaa zilipotimia, tazama! Mapacha walikuwamo tumboni mwake. Wa kwanza akatoka, naye alikuwa mwekundu mwili wote kama vazi la nywele. Wakamwita jina lake Esau. Baadaye ndugu yake akatoka, na mkono wake unamshika Esau kisigino. Akaitwa jina lake Yakobo. Isaka alikuwa mwenye miaka sitini mkewe alipowazaa. Watoto wakakua, Esau alikuwa mtu ajuaye kuwinda wanyama, mtu wa nyikani, na YAKOBO ALIKUWA MTU MTULIVU, mwenye kukaa hemani.”

Mathayo 26:59-63 “Basi wakuu wa makuhani na baraza yote wakatafuta ushuhuda wa uongo juu ya Yesu, wapate kumwua;wasiuone wangawa walitokea mashahidi wa uongo wengi. Hata baadaye wawili wakatokea, wakasema, Huyu alisema, Naweza kulivunja hekalu la Mungu, na kulijenga kwa siku tatu. Kisha Kuhani Mkuu akasimama akamwambia, Hujibu neno? Hawa wanakushuhudia nini? Lakini, YESU AKANYAMAZA. Kuhani Mkuu akamwambia, Nakuapisha kwa Mungu aliye hai, utuambie kama wewe ndiwe Kristo, Mwana wa Mungu.”

Marko 14:55-61 “Basi wakuu wa makuhani na baraza yote wakatafuta ushuhuda juu ya Yesu wapate kumwua; wasione. Kwa maana wengi walimshuhudia uongo, walakini ushuhuda wao haukupatana. Hata wengine wakasimama, wakamshuhudia uongo, wakisema, Sisi tulimsikia akisema, Mimi nitalivunja hekalu hili lililofanyika kwa mikono, na katika siku tatu nitajenga jingine lisilofanyika kwa mikono. Wala hata hivi ushuhuda wao haukupatana. Kisha Kuhani Mkuu akasimama katikati, akamwuliza Yesu, akisema, Hujibu neno? Hawa wanakushuhudia nini? LAKINI AKANYAMAZA, WALA HAKUJIBU NENO. Kuhani Mkuu akamwuliza tena, akamwambia, Wewe ndiwe Kristo, Mwana wake Mtukufu?

Waamuzi 18:7 “Ndipo hao watu watano wakaenda zao, wakafika Laisha, wakawaona wale watu waliokuwamo ndani yake, jinsi walivyokaa salama salimini kwa mfano wa walivyokaa hao Wasidoni, wenye starehe na hifadhi, kwa maana hapakuwa na mtu katika nchi hiyo aliyekuwa na amri, aliyeweza kuwatweza katika neno lo lote, nao walikuwa wa mbali na hao Wasidoni, wala hawakuwa na shughuli na mtu ye yote.”                                

Katika vifungu vya maandiko hapo juu tunaona sasa matumizi na neno kunyamaza. Linavyotumika kwa Yakobo linatumika neno “tām” gentle hii inamaanisha kuwa Yakobo au Israel alikuwa ni mkimya au mtulivu kwa kuzaliwa kwa hiyo kukaa kimya ilikuwa ni tabia yake ambayo kimsingi watoto wake Simoni na Lawi hawakuwahi kukubaliana nayo, waliona ni ukimya unaopelekea hata kuonewa. Binti yake alipobakwa Yakobo alikaa kimya, nahata Reuben alipolala na suria wa baba yake Yakobo alisikia lakini alikaa kimya, kwa hiyo ni wazi kuwa alikuwa ni mtulivu mno upole uliokithiri, utulivu uliopittiliza, alikaa kimya.

Na kwa Bwana Yesu ukimya wake wakati akiwa anashitakiwa mashitaka ya uongo mbele ya mahakama ya kiyahudi yeye alinyamaza “Siōpaō” muteness Ukimya huu ni ukimya wa kupuuzia, au kuamua kupuuzia na kutokutilia maanani maswala ya kipuuzi. Usipoteze muda wako kujibu lolote unalozushiwa ambalo ni la uongo, Yesu watu walipomsingizia na kusema uongo hakujibu lolote alitulia kimya

Na ukimya unaozungumzwa katika andiko kutoka katika kitabu cha waamuzi linazunguiza utulivu wa kukaa kwa amani au bila kusumbuana na maswala ya watu “shākat” yaani “undisturbed” husumbuliwi wala husumbui, hushughuliki na jambo lolote la mtu wala wao hawashughuliki na wewe kwa hiyo unakaa salama kimyaa

Na neno lingine linalotumika katika maandiko ambalo kisingi ndilo tutakalolitumia leo ni neno la kiibrania “Chshh” ambalo maana yake to keep quiet, to hold peace, au to keep silence   Hili ndio linalotumiwa na Roho Mtakatifu kutokumfanya mtu atulie au awe na Amani au anyamaze wakati kuna mzigo ambao Mungu ameuweka ndani yake

Isaya 62:1-3 “Kwa ajili ya Sayuni sitanyamaza, na kwa ajili ya Yerusalemu sitatulia, hata haki yake itakapotokea kama mwangaza, na wokovu wake kama taa iwakayo. Na mataifa wataiona haki yako, na wafalme wote watauona utukufu wako; nawe utaitwa jina jipya, litakalotajwa na kinywa cha Bwana. Nawe utakuwa taji ya uzuri katika mkono wa Bwana, na kilemba cha kifalme mkononi mwa Mungu wako.”


Kwa nini hatuwezi kunyamaza

Roho Mtakatifu anapokuwa ndani yetu, moja ya kazi anayoifanya ni kukutaharakisha, kukupeleka katika kutimiza majukumu ambayo Mungu ameyakusudia na kuyaweka ndani yako, kwa hiyo yeye hukufanya wewe na mimi tusiweze kukaa kimya, Ni kazi ya Roho Mtakatifu kuwatia nguvu waamini na kuwasukuma moyoni kwa kuwanyima Amani, kwa kuwakoseha utulivu, kwa kuwahimiza na kutowafanya wanyamaze mpaka wametimiza kile ambacho Mungu amekikusudia kwa mtu huyo aweze kukitimiza, kwa hiyo Roho wa Mungu anafanyika “Catalyst” kichocheo  ambaye anainua mioyo yetu na kuweka mzigo na moyo na kutuwezesha kusema kile ambacho Mungu amekikusudia ili kitende kazi ndani yetu mfano kama Mungu anaweka neno ndani yetu basi, Roho Mtakatifu anachochea lile neno ambalo Mungu amelikusudia, tuliseme ili tuweze kulisema na inapotokea utaamua kukaa kimya kunatokea changamoto ndani yako zinazokunyima Amani itakayokupelekea ukaseme kila ambacho Mungu amekikusudia ni kwaajili ya Roho Mtakatifu kuweka kitu ndani yako au ndani yangu ndio tunakosa utulivu au uwezo wa kunyamaza “Chshh” kwanini hatuwezi kunyamaza? Ni kwa sababu Roho Mtakatifu haachi kufanya uchochezi ndani yetu!

Yeremia 1:6-8 “Ndipo niliposema, Aa, Bwana MUNGU! Tazama, siwezi kusema; maana mimi ni mtoto. Lakini Bwana akaniambia, Usiseme, Mimi ni mtoto; maana utakwenda kwa kila mtu nitakayekutuma kwake, nawe utasema kila neno nitakalokuamuru. Usiogope kwa sababu ya hao maana mimi nipo pamoja nawe nikuokoe, asema Bwana.”

Ezekiel 33:7-9 “Basi wewe, mwanadamu, nimekuweka kuwa mlinzi kwa nyumba ya Israeli; basi ulisikie neno hili kinywani mwangu, ukawape maonyo yangu. Nimwambiapo mtu mbaya, Ewe mtu mbaya, hakika utakufa, nawe husemi neno la kumwonya mtu huyo, aiache njia yake, mtu mbaya huyo atakufa katika uovu wake, lakini damu yake nitaitaka mkononi mwako. Walakini ukimwonya mtu mbaya kwa sababu ya njia yake, kusudi aiache; wala yeye asiiache; atakufa huyo katika uovu wake, lakini wewe umejiokoa roho yako.”

Kwa hiyo kumbe Mungu anapoweka neno lake au wajibu wake kwa mtumishi Fulani wa Mungu, Roho Mtakatifu huchochea na kumfanya mtu huyo kukosa utulivu mpaka atakapotimiza kile ambacho Mungu amekiweka, matukio ya aina hii yanaweza kuwekwa kwa waombaji, yanaweza kuwekwa kwa wajumbe wa kinabii ambao Mungu anataka wapeleke maonyo na kutia moyo, wajumbe wa kiinjilisti ambao Mungu anawataka waseme habari njema, wajumbe wa kialimu ambao Mungu anawataka wafundishe, wajumbe wa kiandishi ambao Mungu anawataka waandike “haya uyaonayo uyaandike!” , Wajumbe wa kichungaji ambao Mungu anaweka mzigo ndani yao wachunge na kulisha kundi la kondoo wa Bwana, wajumbe wa kitume ambao watapanda makanisa na kuipeleka injili kule Mungu anakotaka, Wajumbe wa kitaaluma ambao Mungu anataka wawake na kupanda taaluma katika jamii, wakati wote Mungu Roho Mtakatifu atawataharakisha watu wake wasikae kimya kwaajili ya kazi zote katika ufalme wa Mungu, yeye huhimiza na kutoa maelekezo kwa kila muhusika kwaajili ya kazi husika ambayo yeye anataka itimizwe

Ezra 5:1-2 “Basi manabii, Hagai nabii, na Zekaria mwana wa Ido, wakawafanyia unabii Wayahudi waliokuwako Yerusalemu na Yuda; waliwafanyia unabii kwa jina la Mungu wa Israeli. Ndipo akaondoka Zerubabeli, mwana wa Shealtieli, na Yoshua, mwana wa Yosadaki, wakaanza kuijenga nyumba ya Mungu iliyoko Yerusalemu; na pamoja nao walikuwa manabii wa Mungu, wakiwasaidia.”

Matendo 8:26-29 “Malaika wa Bwana akasema na Filipo, akamwambia, Ondoka ukaende upande wa kusini hata njia ile itelemkayo kutoka Yerusalemu kwenda Gaza; nayo ni jangwa. Naye akaondoka, akaenda; mara akamwona mtu wa Kushi, towashi, mwenye mamlaka chini ya Kandake malkia wa Kushi, aliyewekwa juu ya hazina yake yote; naye alikuwa amekwenda Yerusalemu kuabudu, akawa akirejea, ameketi garini mwake akisoma chuo cha nabii Isaya. Roho akamwambia Filipo, Sogea karibu na gari hili, ukashikamane nalo.”

Luka 2:25-35 “Na tazama, pale Yerusalemu palikuwa na mtu, jina lake Simeoni, naye ni mtu mwenye haki, mcha Mungu, akiitarajia faraja ya Israeli; na Roho Mtakatifu alikuwa juu yake.Naye alikuwa ameonywa na Roho Mtakatifu ya kwamba hataona mauti kabla ya kumwona Kristo wa Bwana. Basi akaja hekaluni ameongozwa na Roho; na wale wazazi walipomleta mtoto Yesu ndani, ili wamfanyie kama ilivyokuwa desturi ya sheria, yeye mwenyewe alimpokea mikononi mwake, akamshukuru Mungu, akisema,Sasa, Bwana, wamruhusu mtumishi wako, Kwa amani, kama ulivyosema; Kwa kuwa macho yangu yameuona wokovu wako,Uliouweka tayari machoni pa watu wote; Nuru ya kuwa mwangaza wa Mataifa, Na kuwa utukufu wa watu wako Israeli. Na babaye na mamaye walikuwa wakiyastaajabia hayo yaliyonenwa juu yake. Simeoni akawabariki, akamwambia Mariamu mama yake, Tazama, huyu amewekwa kwa kuanguka na kuinuka wengi walio katika Israeli, na kuwa ishara itakayonenewa. Nawe mwenyewe, upanga utaingia moyoni mwako, ili yafunuliwe mawazo ya mioyo mingi   

2Petro 1:20-21 “Mkijua neno hili kwanza, ya kwamba hakuna unabii katika maandiko upatao kufasiriwa kama apendavyo mtu fulani tu. Maana unabii haukuletwa po pote kwa mapenzi ya mwanadamu; bali wanadamu walinena yaliyotoka kwa Mungu, wakiongozwa na Roho Mtakatifu.”                       

Wakati wote Roho Mtakatifu aliwapa uchochezi manabii, mitume na watumishi mbalimbali wa Mungu kuweza kutoa ujumbe, kutabiri na kutia moyo au kuongoza katika haki ili mapenzi ya Mungu yaweze kufahamika na kutendeka katika jamii ya watu ambao Mungu aliwakusudia, Mungu Roho Mtakatifu anapokuwa amekusudia hilo na wewe ndie ambaye umekusudiwa upeleke ujumbe huo basi yeye hatakuacha unyamaze atakusukuma kwa jambo hilo, utaona moto ndani yako, utaona msukumo, utaona kukosa Amani, utaona kusumbuliwa utasikia kushikwa, kukamatwa, kupelekwa kutaharakishwa kuuzishwa mpaka umetenda kile ambacho kimekusudiwa naye


Mifano ya kibiblia ya watu walioshindwa kunyamaza.

Waamuzi 13:24-25 “Basi yule mwanamke akamzaa mtoto mwanamume akamwita jina lake Samsoni, mtoto huyu akakua, Bwana akambarikia. Roho ya Bwana ikaanza kumtaharakisha katika Mahane-dani, katikati ya Sora na Eshtaoli.”

Wote tunafahamu kuwa Samsoni alizaliwa kwa kusudi maalumu, na Mungu alikuwa amemuandaa kuwa mwokozi wa wana wa Israel ambao walikuwa wanaonewa na Wafilisti kwa wakati huo, tunasoma tu kuwa mara baada ya mtoto huyu kukua Roho ya Bwana ikaanza kumtaharakisha maana yake ikamnyima kutulia, ikamnyima kunyamaza Roho Mtakatifu alianza kuweka msukumo na kumfanya ajione hawezi kutulia ni lazima aseme alijiona hawezi kuwa utumwani yeye wala ndugu zake alijisikia kuwa ni lazima afanye kazi yake aliyopewa ya kuwaokoa wana wa Israel kama Jeshi la Mtu mmoja na alikuwa na hisia zilizokuwa zikimuelekeza au kumyima Amani mpaka atafute kisa ili mradi aweze kuwaokoa wana wa Israel, kwa hiyo tunajifunza hapa kuwa Mungu akikupa agizo huwezi kutulia kunakuwepo moto unaokutesa na kukusumbua ukikutaka utimize kusudi ambalo kwa sababu ya hilo ulizaliwa.       

Isaya 58:1-14 “Piga kelele, usiache, Paza sauti yako kama tarumbeta; Uwahubiri watu wangu kosa lao, Na nyumba ya Yakobo dhambi zao. Walakini wanitafuta kila siku; hupenda kujua njia zangu; kama vile taifa waliotenda haki, wasioacha sheria ya Mungu wao, hutaka kwangu amri za haki; hufurahi kumkaribia Mungu. Husema, Mbona tumefunga, lakini huoni? Mbona tumejitaabisha nafsi zetu, lakini huangalii? Fahamuni, siku ya kufunga kwenu mnatafuta anasa zenu wenyewe, na kuwalemea wote watendao kazi kwenu.

Tazama, ninyi mwafunga mpate kushindana na kugombana, na kupiga kwa ngumi ya uovu. Hamfungi siku hii ya leo hata kuisikizisha sauti yenu juu.  Je! Kufunga namna hii ni saumu niliyoichagua mimi? Je! Ni siku ya mtu kujitaabisha nafsi yake? Ni kuinama kichwa kama unyasi, na kutanda nguo za magunia na majivu chini yake? Je! Utasema ni siku ya kufunga, na ya kukubaliwa na Bwana?  Je! Saumu niliyoichagua, siyo ya namna hii? Kufungua vifungo vya uovu, kuzilegeza kamba za nira, kuwaacha huru walioonewa, na kwamba mvunje kila nira?  Je! Siyo kuwagawia wenye njaa chakula chako, na kuwaleta maskini waliotupwa nje nyumbani kwako? Umwonapo mtu aliye uchi, umvike nguo; wala usijifiche na mtu mwenye damu moja nawe? Ndipo nuru yako itakapopambazuka kama asubuhi, na afya yako itatokea mara; na haki yako itakutangulia; utukufu wa Bwana utakufuata nyuma ukulinde. Ndipo utaita, na Bwana ataitika; utalia, naye atasema, Mimi hapa. Kama ukiiondoa nira; isiwepo kati yako, wala kunyosha kidole, wala kunena maovu; na kama ukimkunjulia mtu mwenye njaa nafsi yako, na kuishibisha nafsi iliyoteswa; ndipo nuru yako itakapopambazuka gizani; na kiwi chako kitakuwa kama adhuhuri. Naye Bwana atakuongoza daima, ataishibisha nafsi yako mahali pasipokuwa na maji, na kuitia nguvu mifupa yako; nawe utakuwa kama bustani iliyotiwa maji, na kama chemchemi ambayo maji yake hayapungui.

Na watu wako watapajenga mahali palipokuwa ukiwa; utaiinua misingi ya vizazi vingi; nawe utaitwa, Mwenye kutengeneza mahali palipobomoka; na, Mwenye kurejeza njia za kukalia. Kama ukigeuza mguu wako usihalifu sabato, usifanye anasa yako siku ya utakatifu wangu; ukiita sabato siku ya furaha, na siku takatifu ya Bwana yenye heshima; ukiitukuza, kwa kutokuzifanya njia zako mwenyewe, wala kuyatafuta yakupendezayo, wala kusema maneno yako mwenyewe; ndipo utakapojifurahisha katika Bwana; nami nitakupandisha mahali pa nchi palipoinuka; nitakulisha urithi wa Yakobo baba yako; kwa maana kinywa cha Bwana kimenena hayo.”               

Nabii Isaya aliitwa na Mungu na Mungu alimtaka awaonye wana wa Israel na kuwaeleza kosa lao ili yamkini waweze kutubu, ujumbe wa makemeo wakati mwingine sio ujumbe mwepesi, kama mwanadamu wakati mwingine alisita na au aliingia hofu  na labda alitaka kuacha lakini Roho wa Mungu alimwambia piga kelele wala usiache paza sauti yako kama tarumbeta kwa nguvu onya juu ya unafiki, wa watu wa Mungu, wakati mwingine ni ngumu kuhubiri maneno magumu watu wanaweza kusema ya kuwa unawahukumu na hasa na wewe ukijijua kuwa u mwanadamu hivyo ilikuwa ni sahihi kwa Isaya kusita sita Lakini aliambiwa apige kelele kama tarumbeta awaonye watu, alipaswa kuwa muaminifu kuhubiri ujumbe wote wa Mungu kama ni toba anyooshe, kama ni rehema anyoooshe na asiseme tu maneno laini kama watu walivyokuwa wanataka kwaajili ya hayo Isaya hakunyamaza.

Isaya 58:1 “Piga kelele, usiache, Paza sauti yako kama tarumbeta; Uwahubiri watu wangu kosa lao, Na nyumba ya Yakobo dhambi zao.”

Wakati wote kumbe Roho wa Mungu anapokuwa juu yako kwaajili ya huduma ambayo Mungu ameiweka ndani yako ni ukweli ulio wazi hutatulia, wala hutanyamaza utafanya kile ambacho Mungu amekikusudia, kama ni kuwafungua watu, kama ni kuponya kama ni kujenga mioyo ya watu, kama ni kutangaza habari njema, yeye hatakuacha utulie atataka utangaze kile ambacho Mungu anataka kukifanywa kupitia wewe ilikuwa hivyo kwa Isaya nabii na ilikuwa hivyo kwa Masihi Bwana wetu Yesu.

Isaya 61:1-3 “Roho ya Bwana MUNGU i juu yangu; kwa sababu Bwana amenitia mafuta niwahubiri wanyenyekevu habari njema; amenituma ili kuwaganga waliovunjika moyo, kuwatangazia mateka uhuru wao, na hao waliofungwa habari za kufunguliwa kwao.Kutangaza mwaka wa Bwana uliokubaliwa, na siku ya kisasi cha Mungu wetu; kuwafariji wote waliao; kuwaagizia hao waliao katika Sayuni, wapewe taji ya maua badala ya majivu, mafuta ya furaha badala ya maombolezo, vazi la sifa badala ya roho nzito; wapate kuitwa miti ya haki, iliyopandwa na Bwana, ili atukuzwe.”

Ni maneno ya Nabii Isaya lakini vilevile ni ya Masihi, Yesu alipokuja duniani aliyatumia maneno haya, ni kazi ileile ya Roho Mtakatifu ambaye hataki  mtu mwenye agizo kunyamaza, Roho wa Mungu kupitia Yesu alitaka afungue kinywa chake na kuwahubiria wanyenyekevu habari njema, alitakiwa kuwaganga waliovunjika moyo, alitakiwa kutangaza uhuru kwa mateka, na wafungwa kuwatangazia kufunguliwa, na kuutangaza mwaka wa neema uliokubalika, wasingeliweza kunyamaza kimya katika hayo, na ndio maana tunamuona Yesu akizunguka toka mji mmoja kwenda mji mwingine na vijijini kila mahali akiifanya kazi hii asingeliweza kutulia kwa sababu Roho Mtakatifu alimpaka mafuta kwaajili ya hilo, kila mmoja kwa kusudi lake ambalo kwalo Mungu amekupaka mafuta lifanye kwa bidii na kwa uaminifu wote  na kwa usikivu mkubwa kwa Roho wa Mungu na utaona kuwa huna sababu za kunyamaza!

Isaya 62:1-3 “Kwa ajili ya Sayuni sitanyamaza, na kwa ajili ya Yerusalemu sitatulia, hata haki yake itakapotokea kama mwangaza, na wokovu wake kama taa iwakayo. Na mataifa wataiona haki yako, na wafalme wote watauona utukufu wako; nawe utaitwa jina jipya, litakalotajwa na kinywa cha Bwana. Nawe utakuwa taji ya uzuri katika mkono wa Bwana, na kilemba cha kifalme mkononi mwa Mungu wako.”

Isaya anazungumza kwa niaba ya mji wa Yerusalem yaani Sayuni akimaanisha Israel, kwamba pamoja na kukumbwa na matukio mbalimbali na kubomolewa na maadui lakini haitakuja itokee, mji huu usisimame, ni mji ambao uko kwenye mapenzi ya Mungu, ni mji uliowekewa waombezi, manabii, na waombolezaji maarufu, ambao wanauombea usiku na mchana ili kwamba ufalme wa Mungu uweze kusimama, Kama Mungu alivyomuinua Isaya bado anaendelea kuinua watu wanaoiombea Israel kila iitwapo leo katika kila kona za Dunia, wanaoitakia mema Israel wako kama jeshi, Yerusalem ni mji ambao Utawala halisi wa kimasihi utatawala na Kristo akiwa Mfalme wa utawala huo Wakristo wanapoomba katika sala ya Bwana ufalme wako uje na mapenzi ya Mungu yatimizwe hapa duniani kama mbinguni Mathayo 6:10 maana yake tunaomba pia kwamba Yesu arudi na kusimamisha utawala wake hapa duniani na ufalme huo na kiti chake cha Enzi kitakuwa Israel,Pale Yerusalem, Sayuni, Kwaajili ya Israel Hatuwezi kunyamaza

Yeremia 20:7-9 “Ee Bwana, umenihadaa, nami nimehadaika; wewe una nguvu kuliko mimi, ukashinda; nimekuwa kitu cha kuchekesha, mchana kutwa; kila mtu hunidhihaki.Maana kila ninenapo napiga kelele, nalia, Dhuluma na uharibifu! Kwa kuwa neno la Bwana limefanywa shutumu kwangu, na dhihaka, mchana kutwa. Nami nikisema, Sitamtaja, wala sitasema tena kwa jina lake; basi, ndipo moyoni mwangu kumekuwamo kama moto uwakao, uliofungwa ndani ya mifupa yangu, nami nimechoka kwa kustahimili, wala siwezi kujizuia.”             

Yeremia alitumwa na Mungu kumbuka kuwa Mungu aliweka maneno ndani yake na kumuamuru kuyasema haikuwa kitu rahisi kukubalika katika mioyo ya watu kiasi ambacho hata pamoja na kuwa Mungu alimwambia nitakuwa pamoja naye alikutana na magumu sana alitiwa gerezani, aliteswa alitupwa katika shimo  la matope ilifikia hatua alitaka kukaa kimya asiseme lakini kwa kadiri alivyokuwa akijitahidi akae kimya kuna nguvu ya kiungu iliyokuwa inamlazimisha kusema wivu wa kiungu ulijaa ndani yake na alipoona uovu uliokuwa ukiendelea na ujumbe aliopewa kusema maneno yalimuunguza akawa hawezi kuyafumbia mdomo alilazimika kutangaza kile ambacho Mungu alikuwa amemuagiza pamoja na kuwa ilimgharimu mateso makali na maumivu makubwa.

Yeremia 47:6-7 “Ee upanga wa Bwana, Siku ngapi zitapita kabla hujatulia? Ujitie katika ala yako; Pumzika, utulie.Utawezaje kutulia, Ikiwa Bwana amekupa agizo? Juu ya Ashkeloni na juu ya pwani, Ndipo alipoyaamuru hayo.”

Wafilisti walikuwa wanaikalia pwani ya Yuda na mara nyingi kihistoria kulikuwa na ugomvi kati ya nchi ya Israel na wafilisti,  Yeremia alitakiwa kutoa unabii wa kuwaonya wafilisti ya kuwa upanga wa Bwana utawahusu, ni kama Mungu alikuwa ameamuru hukumu kwa wafilisti kuwa upanga wa Bwana uipige Gaza na Ashkeloni, ilionekana kuwa hakutakuwa na utulivu kwa wafilisti, kila wakati Gaza itapigwa, hatujui kama nabii aliwaombea wafilisti angalau upanga utulie Lakini lilikuwa ni agizo la Mungu upanga ulikataa kutulia kwa sababu ulikuwa na agizo la Mungu, utawezaje kutulia ikiwa Bwana amekupa agizo? Kupigwa kwa Gaza ni agizo la kimaandiko na itaendelea kuwa hivyo kwa sababu ndivyo neno la Mungu linavyosema na Roho wa Mungu husukuma hukumu juu ya Gaza kwa sababu ni agizo lililoko katika neno lake.

Yoel 2:28-29 “Hata itakuwa, baada ya hayo, ya kwamba nitamimina roho yangu juu ya wote wenye mwili; na wana wenu, waume kwa wake, watatabiri, wazee wenu wataota ndoto, na vijana wenu wataona maono; tena juu ya watumishi wenu, wanaume kwa wanawake, katika siku zile, nitamimina roho yangu.”

Ni unabii wa maana sana kimsingi unahusiana na siku za mwisho na ujio wa Roho Mtakatifu kama alivyoona Yoel Roho Mtakatifu atakuja na kazi maalumu kwa kila watu na makundi na kila mmoja hataweza kukaaa kimya atasema tu, watatabiri, wanaona maono, wataota ndoto, kwa hiyo tunaweza kukubaliana wote ya kuwa ubatizo wa Roho Mtakatifu utasababisha na kumfanya kila mwanadamu kutokutulia, neno la Mungu linasema tena juu ya watumishi wangu, nini maana yake watumishi maana yake “Bond Servants” ni neno limetumika mara 800 katika maandiko likimaanisha ni watu wa kazi watumwa hawatatulia, kila atakayepewa Roho wa Mungu hataweza kuwa na utulivu atafanya kile ambacho Mungu ambaye ni bwana wetu amekusudia akifanye.  

Mika 3:8 “Bali mimi, hakika nimejaa nguvu kwa roho ya Bwana; nimejaa hukumu na uwezo; nimhubiri Yakobo kosa lake, na Israeli dhambi yake.”

Mika aliitwa kuwa msemaji kwa niaba ya Mungu yaani nabii, alinena kwa uweza wa Roho Mtakatifu, alitakiwa kuikemea dhambi katika nyumba ya Mungu na ilikuwa ni kazi aliyopewa pamoja na kuonyesha moyo wa Mungu, kutia moyo na kukatisha tamaa uovu, wakati wa Mika kulikuwa na manabii wa uongo wengi, waliokuwa wakiwakosesha watu wa Mungu kwa jumbe zisizo za kweli, lakini uweza wa Roho wa Bwana haukumpa Amani Mika alipewa kusema, alipewa kuonya, alipewa kutangaza hukumu, alipewa kutangaza rehema asingeliweza kunyamaza

Mika 3:5 “Bwana asema hivi katika habari za manabii wanaowakosesha watu wangu; hao waumao kwa meno yao, na kulia, Amani; na mtu awaye yote asiyetia kitu vinywani mwao, wao humwandalia vita.”

Mungu alimtaka Mika kukemea na kusema kweli, bila kujali kuwa liko kundi la manabii feki yaani wa uongo, Kanisa halipaswi kufuata shinikizo la watu Fulani ndani au nje ya nchi wanaotaka tuwe na mtindo Fulani unaofanana wa maisha hata kama mambo hayo ni uovu yako kinyume na Mungu na mila zetu, Kanisa ni lazima likemee bila huruma kile ambacho kinaonekana kuwa ni uongo na kuwa kiko kinyume na mapenzi ya Mungu, Mika hakufuata mkumbo alibaki katika zamu yake na kukemea kweli kweli kwa sababu nyuma yake kulikuwa na shinikizo la Roho Mtakatifu kwanini hatuwezi kunyamaza kwa sababu Roho wa Mungu anafanya hivyo ndani yetu, hakuna anayeweza kutulia!

Zekaria 4:6-9 “Akajibu akaniambia, akisema, Hili ndilo neno la Bwana kwa Zerubabeli, kusema, Si kwa uwezo, wala si kwa nguvu, bali ni kwa roho yangu, asema Bwana wa majeshi.Nani wewe, Ee mlima mkubwa? Mbele ya Zerubabeli utakuwa nchi tambarare; naye atalileta lile jiwe la kuwekwa juu kabisa pamoja na vigelegele vya, Neema, neema, ilikalie. Tena neno la Bwana likanijia, kusema, Mikono yake Zerubabeli imeiweka misingi ya nyumba hii, na mikono yake ndiyo itakayoimaliza; nawe utajua ya kuwa Bwana wa majeshi amenituma kwenu.”

Mungu alimuinua Zerubabeli kuijenga tena Nyumba ya Mungu katika mazingira magumu wakati Israel waliporejea kutoka utumwani Babeli yaani wayahudi, kazi hii ilikuwa ngumu kiasi ambacho kuna wakati watu walikuwa kama wameisusia, Lakini Mungu aliwainua manabii Habakuki, Zekaria na Malaki kuwatia moyo viongozi waliokuwa wanahusika na agizo la kuijenga nyumba ya Bwana walipokuwa wanasita sita Zekaria alipewa ujumbe kumtia Moyo Zerubabeli kuwa nyumba hiyo itajengeka tu sio kwa uweza wa kiserikali wala wa kijeshi bali Roho Mtakatifu, huyu atainua hari ya wajenzi na watajenga kwa uwezo wake hakuna mtu atakayeweza kutulia kwa sababu Roho wa Mungu atasababisha kazi yake itendeke na hakuna kikwazo chochote kitakachoweza kusimama mbele ya wajenzi.

Matendo 1:8 “Lakini mtapokea nguvu, akiisha kuwajilia juu yenu Roho Mtakatifu; nanyi mtakuwa mashahidi wangu katika Yerusalemu, na katika Uyahudi wote, na Samaria, na hata mwisho wa nchi.”    

Ni tangazo la ujio wa Roho Mtakatifu kwa kanisa, mitume waliagizwa kusubiria ubatizo huo na walihakikishiwa kuwa watakapopokea ubatizo wa Roho Mtakatifu hawataweza kukaa kimya watasema, watahubiri, watathibitisha na kuwa wao ni mashahidi wa kweli kwaajili ya Yesu kristo, hatakuja kuwa na kizuizi watamtii Mungu kuliko wanadamu katika swala zima la kuhubiri injili.

Matendo 5:17-32 “Akaondoka Kuhani Mkuu na wote waliokuwa pamoja naye, (hao ndio walio wa madhehebu ya Masadukayo), wamejaa wivu, wakawakamata mitume wakawaweka ndani ya gereza; lakini malaika wa Bwana akafungua milango ya gereza usiku, akawatoa, akasema, Enendeni mkasimame hekaluni mkawaambie watu maneno yote ya Uzima huu. Nao waliposikia wakaenda alfajiri hekaluni, wakaanza kufundisha. Akaja Kuhani Mkuu nao waliokuwa pamoja naye, wakawakutanisha watu wa baraza, na wazee wote wa wana wa Israeli, wakatuma watu gerezani ili wawalete. Hata watumishi walipofika hawakuwaona gerezani, wakarudi wakatoa habari, wakisema, Gereza tumeikuta imefungwa salama, nao walinzi wamesimama mbele ya mlango; lakini tulipoufungua hatukukuta mtu ndani. Basi jemadari wa hekalu na wakuu wa makuhani waliposikia haya, wakaingiwa na shaka kwa ajili yao, litakuwaje jambo hilo. Mtu mmoja akaja akawapasha habari ya kwamba, Watu wale mliowaweka gerezani wako ndani ya hekalu, wamesimama wakiwafundisha watu. Ndipo yule jemadari akaenda pamoja na watumishi, wakawaleta, lakini si kwa nguvu, kwa maana waliogopa watu wasije wakawapiga kwa mawe. Walipowaleta, wakawaweka katika baraza. Kuhani Mkuu akawauliza, akisema, Je! Hatukuwaamuru ninyi kwa nguvu, msifundishe kwa jina hili? Nanyi, tazameni, mmeijaza Yerusalemu mafundisho yenu, na mnataka kuileta damu ya mtu yule juu yetu. Petro na mitume wakajibu, wakisema, Imetupasa kumtii Mungu kuliko wanadamu. Mungu wa baba zetu alimfufua Yesu, ambaye ninyi mlimwua mkimtundika katika mti. Mtu huyo Mungu amemtukuza kwa mkono wake wa kuume, awe Mkuu na Mwokozi, awape Waisraeli toba na msamaha wa dhambi. Na sisi tu mashahidi wa mambo haya, pamoja na Roho Mtakatifu ambaye Mungu amewapa wote wamtiio.”

Mitume walikuwa na agizo la kuihubiri injili, na Mungu Roho Mtakatifu alikuwa amewabatiza kusudi waweze kulitimiza kusudi hilo pana la Mungu, hata hivyo walikutana na upinzani mkali kutoka kwa wazee wa kiyahudi wajulikanao kama Sanhedrin yaani mahakama kuu ya kiyahudi, hawa waliwakataza wasihurbiri wala wasiseme kitu kuhusu Yesu, waliwatia gerezani lakini hata hivyo malaika wa Bwana aliwafungulia hawawezi kunyamaza waliagizwa waendelee kufundisha na walifanya hivyo, wazee walikasirika sana  wakiwataka wakae kimyaa Petro  na mitume wakajibu hoja kuwa imetupasaa kumtii Mungu kuliko wanadamu, Roho Mtakatifu hutuwezesha kuwa na utii wa kiwango cha juu kwaajili ya kile ambacho tumeitiwa kukifanya na kufundisha na kulisema neno lake tunawezaje kunyamaza? Kanisa ndio maana hatuwezi kunyamaza na ndio maana hata mimi na wewe hatuwezi kunyamaza.    

Matendo 17:16 “Paulo alipokuwa akiwangojea huko Athene na kuona jinsi mji ule ulivyojaa sanamu, roho yake ilichukizwa sana ndani yake.”

Paulo mtume aliihubiri injili huko Thesalonike na Beroya, hata hivyo wayahudi wenye wivu walimuwinda na kutaka kumua, kwa hiyo wanafunzi waliookoka walimpeleka Paulo katika mji wa Athene ili awasubiri Timotheo na Sillas ambao walibaki katika miji ya awali, Neno la Mungu linatuambia  wakati alipokuwa akiwasubiri huko Athene aliona mji ule umejaa sanamu, roho yake ilichukizwa sana Katika kiingereza tunaambiwa hivi “his spirit was stirred in him” neno stirred katika kiyunani ni “Paroxunō” maana yake easily Provoked  yaani alichochewa, alipatwa na hasira ya kiungu au alisukumwa kutokukaa kimya, Roho Mtakatifu ndani ya Paulo mtume alipoona sanamu hakusubiri aliona itachelewesha akaanza kuhubiri, Roho wa Mungu hatakuacha unyamaze akiwa ameweka kitu au mzigo au wajibu ambao unatakiwa uutekeleze. Je wewe roho yako inachukizwa? Unapoona wanadamu wanaoana na mbwa? unachukizwa na kuona mwanaume akimpa binti yake mimba?, wanadamu wakilala na wanyama, madaktari wakifanya ngono na wagonjwa, watumishi wanapozini na washirika, matajiri wakipewa nafasi ya vyeo vikubwa makanisani, washirika wakiibiwa fedha na kutajirisha wahubiri, Wahubiri wakijilimbikizia mali, kampeni za kisiasa zikitapakaa makanisani, watu wakipeana sumu kwaajili ya nafasi za uongozi, watu wakiombewa bila kuongozwa sala ya toba, wanakwaya wakitembea wenyewe kwa wenyewe, wanamuziki wakiacha waume zao na ndoa zao kwa kisingizio cha wito, unanyamazaje wakati utoaji wa mimba umeingia makanisani hata wanandoa waliookoka siku hizi wanatoa mimba?, madawa ya kuleywa yakiuzwa kila mahali, rushwa na ushoga umetapakaa kila mahali, unanyamazaje wakati watu wakiwa wahanga wa picha za ngono? Uamsho ukisisitizwa bila utakatifu, mafundisho potofu yakiwa hayakemewi, watu wakiwa wanatekwa na kuuawa, mauaji ya kutisha yakisambaa, ulawiti na ubakaji uliokithiri, hali ya uchumi ikiendelea kuwa mbaya? Paulo mtume angekuwepo leo asingeliweza kunyamaza, ikiwa sanamu tu zilimsumbua sana sisi nasi hatunabudi kuhakikisha kuwa tunaifikia jamii na kuijenga kwa gharama yoyote ile na kamwe hatuwezi kunyamaza!, Roho Mtakatifu akiwa ndani yetu roho zetu zitachukizwa hatuwezi kunyamaza!

Warumi 1:16-17 “Kwa maana siionei haya Injili; kwa sababu ni uweza wa Mungu uuletao wokovu, kwa kila aaminiye, kwa Myahudi kwanza, na kwa Myunani pia. Kwa maana haki ya Mungu inadhihirishwa ndani yake, toka imani hata imani; kama ilivyoandikwa, Mwenye haki ataishi kwa imani.”                

Paulo mtume anaonyesha wazi kuwa haionei haya injili kwa sababu ni uweza wa Mungu uletao wokovu kwa watu waaminio, kutokana na uwezo mkubwa wa habari njema kuwasaidia wanadamu na kuwapa uzima wa milele bure kwa Imani katika Kristo Yesu Paulo anaona ana wajibu wa kutokuionea haya injili iwe ni kwa kufungwa au kudhaliliswa, au kuteswa kwa sababu zozote zile hawezi kuona aibu kwa sababu ya injili, maana yake pia hawezi kukaa kimya kwaajili ya injili ataendelea kuisema katika mazingira yoyote.

2Timotheo 1:7-9 “Maana Mungu hakutupa roho ya woga, bali ya nguvu na ya upendo na ya moyo wa kiasi.Basi usiuonee haya ushuhuda wa Bwana wetu, wala usinionee haya mimi mfungwa wake, bali uvumilie mabaya pamoja nami kwa ajili ya Injili, kwa kadiri ya nguvu ya Mungu; ambaye alituokoa akatuita kwa mwito mtakatifu, si kwa kadiri ya matendo yetu sisi, bali kwa kadiri ya makusudi yake yeye na neema yake. Neema hiyo tulipewa katika Kristo Yesu tangu milele,”

Paulo anamkumbusha Timotheo kutokuonea haya ushuhuda wa Bwana, kutokuionea haya ufungwa kwaajili ya injili, anamtaka avumilie mabaya kwaajili ya injili aendelee kwa kadiri ya nguvu za Mungu aliyewaita akimkumbusha kuwa Roho Mtakatifu sio Roho ya woga bali ni ya nguvu na upendo na moyo wa kiasi kwa hiyo haijalishi ni magumu kiasi gani anakutana nayo anamtaka aendelee na kazi ya wito mtakatifu kwa kusudi lile kuu, Roho Mtakatifu huondoa woga wote na kutupa ujasiri, na nguvu na upendo ili tuweze kusonga mbele kwa wito tulioitiwa hivyo hatuwezi kunyamaza, Ni yeye ambaye akiwa ndani yetu tutavurugwa, tutachukizwa na sanamu, tutataharakishwa hatutakubali uonevu wa ibilisi dhidi ya ndugu zetu, tutawaombea watu, tutawafungua watu, tutawapa watu mahitaji yao kwa msukumo wa Roho Mtakatifu ndani yetu ni yeye ni yeye ni yeye anayesababisha hatuwezi kunyamaza kamwe!

2Timotheo 2:8-9 “Mkumbuke Yesu Kristo, aliyefufuka katika wafu, wa uzao wa Daudi kama inenavyo injili yangu. Nami katika hiyo nimeteswa hata kufungwa kama mtenda mabaya; lakini neno la Mungu halifungwi.”

Mwisho Paulo mtume akiwa kifungoni anamkumbusha Timotheo kumkumbuka Yesu aliyefufuka katika wafu, ya kuwa uko ushindi katika maisha yetu ya kazi ya injili kama Daudi alivyoshinda Vita vyote kwa jinsi ya mwili, Yesu naye ameshinda vita vyote vya kiroho, kwa hiyo hata ingawa Paulo mtume alikuwa kifungoni, alimwambia Timotheo kuwa neno la Mungu halifungwi, akiwa kifungoni hakuweza kunyamaza na badala yake alianza kuandika nyaraka zenye kuwatia moyo waamini na watumishi wa Mungu na kuendelea kuwajenga, Katika nyakati zetu leo hata kama tutakuwa gerezani, injili itaendelea kwa sababu Roho Mtakatifu hatatuacha kunyamaza. Neno la Mungu halifungwi! Roho Mtakatifu hatatuacha tuwe na utulivu bila kutimiza ile huduma ya upatanisho aliyoiweka ndani yetu haleluyaa!

Hitimisho

Usinyamaze kwaajili ya kile ambacho Mungu amekuitia kukifanya uwepo wa Roho Mtakatifu katika maisha yetu unatufanya kuwa na msaidizi wa karibu ndani yetu, kiongozi ndani yetu, mwenye kututia nguvu, na anatutia nguvu na kutupa nguvu za ushawishi ndani yetu, Hatuna budi kumtii  na kukubali kuongozwa naye katika kuyatii mapenzi yake na tunapomtii atasema nasi na kutusukuma kama nguvu ya moto ndani yetu akiweka wivu, wa Bwana na kutusukuma katika kuyatii mapenzi yake kwa hiyo ni lazima kuhakikisha kuwa tunaihubiri injili kwa namna yoyote kila mmoja kwa kadiri ya wito wake alioitiwa na kamwe tusiache kwa sababu tukiacha watu watakengeuka, mwenye kuomba asiache kuomba, mwenye kuhubiri asinyamaze, mwenye kutoa asiache, mwenye kuangalia wafungwa asiache, mwenye kufariji wajane na yatima asiache, mwenye kushuhudia asiache, mwenye kufundisha asiache mwenye kusimamia asiache, mwenye kutia moyo asiache na mwenye kuandika kama mimi asiache hakuna anayeweza kutunyamazisha kwa sababu Roho wa Mungu anataka kila kitu kitimizwe ndani yetu kwa wakati wake! 

2Timotheo 4:1-5 “Nakuagiza mbele za Mungu, na mbele za Kristo Yesu, atakayewahukumu walio hai na waliokufa; kwa kufunuliwa kwake na kwa ufalme wake; lihubiri neno, uwe tayari, wakati ukufaao na wakati usiokufaa, karipia, kemea, na kuonya kwa uvumilivu wote na mafundisho. Maana utakuja wakati watakapoyakataa mafundisho yenye uzima; ila kwa kuzifuata nia zao wenyewe watajipatia waalimu makundi makundi, kwa kuwa wana masikio ya utafiti;nao watajiepusha wasisikie yaliyo kweli, na kuzigeukia hadithi za uongo.Bali wewe, uwe na kiasi katika mambo yote, vumilia mabaya, fanya kazi ya mhubiri wa Injili, timiliza huduma yako.”

Warumi 12:4-8 “Kwa kuwa kama vile katika mwili mmoja tuna viungo vingi, wala viungo vyote havitendi kazi moja; Vivyo hivyo na sisi tulio wengi tu mwili mmoja katika Kristo, na viungo, kila mmoja kwa mwenzake. Basi kwa kuwa tuna karama zilizo mbalimbali, kwa kadiri ya neema mliyopewa; ikiwa unabii, tutoe unabii kwa kadiri ya imani; ikiwa huduma, tuwemo katika huduma yetu; mwenye kufundisha, katika kufundisha kwake; mwenye kuonya, katika kuonya kwake; mwenye kukirimu, kwa moyo mweupe; mwenye kusimamia kwa bidii mwenye kurehemu, kwa furaha.”

Roho wa Mungu hututia nguvu katika maisha yetu kuishinda aibu, woga, na vikwazo na kutupa ujasiri na hali ya kutokuweza kukaa kimya akitenda kazi ndani yetu na kututia nguvu na ujasiri na kutuagiza kwa neno lake na kwa sababu hiyo hatuwezi kunyamaza, Martini Luther King Jr alikuwa mchungaji lakini wakati huo ulikuwa ni wakati wa ubaguzi mkubwa wa rangi nchini Marekani, alisimama sio tu kama Muhubiri lakini aliionyesha jamii kuwa matukio ya kibaguzi sio kitu sahihi, hakunyamaza kila lilipojitokeza tukio la kibaguzi na aliuawa kwaajili ya hilo, naamini kuwa Mungu alimtia nguvu, kutokukaa kimya na yeye alisema tutakaa kimya pale tu tutakapokuwa tumekufa, au kwa lugha nyingine Maisha yetu hufikia mwisho pale tu tunapoanza kukaa kimya kwaali ya maswala ya msingi Our lives begin to end the day we become silentBill Bright yeye alisema “Why we cannot remain Silence  kwanini hatuwezi kukaa kimya akikazia kwa sababu tuna agizo kuu la kuihubiri injili, na mimi nimesema kwanini hatuwezi kunyamaza kwa sababu Roho Mtakatifu yuko ndani yetu naye ndiye kichocheo na sababu kwanini hatuwezi kunyamaza.

Wewe nawe kamwe usikae kimya kwa kile ambacho Roho Mtakatifu amekuwekea ndani yako,  Endelea kupiga kelele kama ni za uamsho, kemea kama ni za kukemea manabii wa uongo, kama ni injili ihubiri, unazo sababu lukuki kwanini hauwezi kukaa kimya, tunazo sababu nyingi kwanini hatuwezi kunyamaza haleluyaaa! Uongezewe neema

Rev. Innocent Samuel Kamote

Mkuu wa wajenzi mwenye Hekima   

Jumanne, 17 Septemba 2024

Msaidizi Mwingine!


Yohana 14:16-18 “Nami nitamwomba Baba, naye atawapa Msaidizi mwingine, ili akae nanyi hata milele; ndiye Roho wa kweli; ambaye ulimwengu hauwezi kumpokea, kwa kuwa haumwoni wala haumtambui; bali ninyi mnamtambua, maana anakaa kwenu, naye atakuwa ndani yenu. Sitawaacha ninyi yatima; naja kwenu.”



Utangulizi:

Leo tutachukua Muda tena kujifunza kwa kina na mapana na marefu, tukikazia tena na tena umuhimu wa Mungu Roho Mtakatifu katika maisha yetu, Ambaye Bwana Yesu alimuita Msaidizi mwingine, kanisa ni muhimu sana sana kufahamu na kutoa nafasi kwa Roho Mtakatifu kwa sababu yeye ni msaada mkubwa sana wa kutuondolea mashaka na kutupa neema ya kuishi kwa Amani.

Yohana 14:16-18 “Nami nitamwomba Baba, naye atawapa Msaidizi mwingine, ili akae nanyi hata milele; ndiye Roho wa kweli; ambaye ulimwengu hauwezi kumpokea, kwa kuwa haumwoni wala haumtambui; bali ninyi mnamtambua, maana anakaa kwenu, naye atakuwa ndani yenu. Sitawaacha ninyi yatima; naja kwenu.”

Wanafunzi wa Bwana wakiwa pamoja naye katika karamu yake ya mwisho pamoja nao. Yesu anawaeleza kuwa amekamilisha kazi aliyotumwa na baba na kuwa kilele cha kazi aliyotumwa ni kufa msalabani kwaajili ya wengi, wanafunzi waliposikia kuwa Yesu anazungumza maswala mengi yanayohusu kuhitimisha huduma yake duniani, walipata mashaka na huzuni nyingi, walifadhaika na kujiona kupwaya na kuwa dhaifu, itakuwaje maisha yao bila Yesu?, nani atakuwa pamoja nao, nani atawasaidia, nani atawashauri, nani atakuwa karibu nao, nani atawatia moyo, nani atawafundisha na kuwaelekeza, na wanawezaje kuukabili ulimwengu ambao ni mgumu bila msaada wa Mungu, kukabiliana na wakuu wa dini za kiyahudi, kukabiliana na upinzani wa kiimani na kidhehebu, watu wenye kuipinga injili na habari za Mungu, akijua kila kilichokuwa kinaendelea katika mioyo yao, Yesu aliwathibitishia kuwa atamuomba baba naye atawapa msaidizi mwingine ili akae nasi milele.

Roho Mtakatifu ndiye Msaidizi huyo, Roho Mtakatifu ni wa Muhimu sana sana katika maisha yetu, hakuna lugha ya kuweza kuelezea vya kutosha lakini ikiwa Yesu anasema yafaa au yatufaa au yawafaa yeye aondoke kwa kuwa asipoondoka msaidizi hatakuja kwetu, maana yake Msaidizi huyu ni wa Muhimu na msaada ulio karibu zaidi tukinena kiwazimu kuliko uwepo wa Yesu Kristo duniani, Uwepo wa Yesu Kristo duniani akiwa kama mwanadamu ulimfunga na kumpa mipaka ya kuwepo katika inchi ya Israel tu, vilevile kutokuweza kukaa moyoni mwa kila muumini, Lakini uwepo wa Roho Mtakatifu ambaye hayuko katika mwili, unamuwezesha kuwepo kila mahali na kuwepo ndani ya moyo wa kila aaminiye na kutimiza mambo makubwa sana katika kiwango kile kile alichokuwa anakifanya Yesu Duniani kwa uweza wa Roho Mtakatifu, Ndio maana Yesu akasema yafaa yeye aende, ili Roho Mtakatifu aweze kuchukua nafsi na kukaa nasi hata milele unaona ?

Yohana 16:6-7 “Ila kwa sababu nimewaambia hayo huzuni imejaa mioyoni mwenu. Lakini mimi nawaambia iliyo kweli; yawafaa ninyi mimi niondoke, kwa maana mimi nisipoondoka, huyo Msaidizi hatakuja kwenu; bali mimi nikienda zangu, nitampeleka kwenu.”

Neno yawafaa, au yafaa Katika kiingereza linatumika neno expedient ambalo kwa kiyunani linasomeka kama Sumpherō ambalo tafasiri yake kwa kiingereza ni to be good, Be profit, be profitable, be better yaani kwa Kiswahili, yafaa, ni afadhali, ni faida, ni vema zaidi, ni bora zaidi kwa hiyo kuondoka kwa Yesu ni bora zaidi, ili aje Roho Mtakatifu kuliko kuendelea kuweko kwa Yesu Duniani, katika jinsi ya mwili, ikiwa Yesu aliona umuhimu wa swala hili basi kanisa ni muhimu kwetu kuelewa kuwa Yesu alikuwa Mwalimu bora zaidi kuliko wote duniani, ni mwafalasafa mkubwa zaidi kuliko wote, ni mtenda miujiza mikubwa kuliko mtu awaye yote duniani ana sifa ambazo hakuna mwanadamu awaye yote anazo duniani lakini anasema ni afadhali yeye aende kuliko kubaki ili aje Roho Mtakatifu ambaye ndiye msaidizi, basi kuna umuhimu mkubwa sana wa kulizingatia hili, kwa sababu hiyo leo tutachukua muda kujifunza kwa kina na mapana na marefu somo hili muhimu Msaidizi mwingine kwa kuzingatia vipengele vitatu vifuatavyo:-

·         Msaidizi mwingine.

·         Umuhimu wa kuwa na Msaidizi mwingine.

·         Jinsi ya kuwa na msaidizi mwingine.     

Msaidizi mwingine

Yohana 14:16-18 “Nami nitamwomba Baba, naye atawapa Msaidizi mwingine, ili akae nanyi hata milele; ndiye Roho wa kweli; ambaye ulimwengu hauwezi kumpokea, kwa kuwa haumwoni wala haumtambui; bali ninyi mnamtambua, maana anakaa kwenu, naye atakuwa ndani yenu. Sitawaacha ninyi yatima; naja kwenu.”

Msaidizi mwingine anayetajwa katika maandiko haya ni Roho Mtakatifu, neno Msaidizi mwingine katika kiingereza linatumika kama neno “Another Comforter” ambalo kimsingi katika kiyunani linasomeka kama Parakletōs  ambalo katika kiingereza tafasiri zake ni Consoler, an intercessor, advocate, tafasiri zake one called to the side of another for the purpose of helping him in any way Kwa Kiswahili sasa maana ya Msaidizi mwingine ni Mfariji, mtetezi, mwanasheria, wakili, rafiki, na mshauri, Kwa hiyo ni wazi kuwa Yesu anamuelezea Roho Mtakatifu kama nafsi nyingine itakayosimama kwa niaba ya kanisa na kuwatetea, kuwafariji, kuwatia nguvu, kuwashauri na kuwapa cha kusema au kusema kwa niaba yao hata wanapokuwa katika kumbi za kimahakama, au katika mabaraza na mbele ya maliwali, Roho Mtakatifu atakuwa kama wakili wakati huo. Na sio wakili atakayehitaji malipo bali anayefanya hivyo kwa sababu ya upendo wake Mungu, na kuwashauri watu wake kipi cha kutamka na kwa jinsi gani watamke na kuwashinda wale wanaowashambulia, Biblia ya kiingereza the Amplified Bible inatumia maneno haya katika kiingereza  And I will ask the Father, and he will give you another Helper (comforter, Advocate, Intercessor, Counselor, Strengthener, standby ) to be with you forever ” na Biblia ya kiaramu the Aramaic Bible inasema hivi katika kiiingereza “ And I shall request from my Father and he will give you another Redeemer of the accursed, that he will be with you for eternity” kwa hiyo Roho Mtakatifu ni Mfariji, ni wakili, ni muombezi, ni kiongozi, ni mtia moyo, ni msaada ulio karibu, Roho Mtakatifu ni Mkombozi mwingine dhidi ya mshitaki wetu. Kwa hiyo Roho Mtakatifu ambaye atakaa ndani yetu atatusaidia kutimiliza kile kile ambacho Kristo angetenda akiwa pembeni yetu.

Mathayo 10:17-20 “Jihadharini na wanadamu; kwa maana watawapeleka mabarazani, na katika masinagogi yao watawapiga; nanyi mtachukuliwa mbele ya maliwali na wafalme kwa ajili yangu, kuwa ushuhuda kwao na kwa mataifa. Lakini hapo watakapowapeleka, msifikiri-fikiri jinsi mtakavyosema; maana mtapewa saa ile mtakayosema. Kwa kuwa si ninyi msemao, bali ni Roho wa Baba yenu asemaye ndani yenu.”

Matendo 6:8-10 “Na Stefano, akijaa neema na uwezo, alikuwa akifanya maajabu na ishara kubwa katika watu. Lakini baadhi ya watu wa sinagogi lililoitwa sinagogi la Mahuru, na la Wakirene, na la Waiskanderia, na la wale wa Kilikia na Asia, wakaondoka na kujadiliana na Stefano;lakini hawakuweza kushindana na hiyo hekima na huyo Roho aliyesema naye.”

Katika lugha ya kiebrania neno hilo Msaidizi linatajwa kama neno “Ezer” ambalo maana yake ni Msaada au msaada ulio karibu kwa hiyo Roho Mtakatifu ni Msaada ulio karibu, ni msaada wa kimwili na kiroho  na kihekima na kiushauri na kimuelekeo, na kiuaffanuzi, na kiualimu, na hutusaidia katika udhaifu wetu, hutusaidia na kututia nguvu wakati wa mateso na kutuongoza katika kweli yote, Kimsingi Roho wa Mungu ni msaada kamili kama ule tu ambao ungepatikana kwa Mungu baba na Mungu mwana yaani Yesu kristo. Roho Mtakatifu ndani yetu katika roho ni muhimu kuliko Yesu Kristo pembeni yetu katika mwili.

Zaburi 46:1-2 “Mungu kwetu sisi ni kimbilio na nguvu, Msaada utakaoonekana tele wakati wa mateso. Kwa hiyo hatutaogopa ijapobadilika nchi, Ijapotetemeka milima moyoni mwa bahari.”

Warumi 8:26 “Kadhalika Roho naye hutusaidia udhaifu wetu, kwa maana hatujui kuomba jinsi itupasavyo, lakini Roho mwenyewe hutuombea kwa kuugua kusikoweza kutamkwa.”

Kwa hiyo Roho Mtakatifu ni msaada wa karibu katika kutoa ushauri wa hekima, ushauri wa nini cha kusema, kipi cha kufanya, anazungumza kwa niaba yetu, anashughulika kwa niaba yetu, anatutia nguvu, anatupa wepesi anatusaidia wakati wa majaribu na wakati wa mambo magumu, na wakati wa mateso, na wakati wa hatari, na wakati wa upinzani, kwa maana nyingine msaada ule ule aliokuwa akiutoa Yesu Kristo alipokuwa Duniani pamoja na wanafunzi wake, ndio msaada anaoutoa Roho Mtakatifu kwa kila mwamini kokote aliko, na msaada ule ule anaoutoa Mungu baba tunaupata kwa Roho Mtakatifu akaaye ndani yetu, kwa hiyo utaweza kuona umuhimu wake katika maisha yetu

Ni muhimu vile vile kufahamu kuwa neno Msaidizi mwingine yaani neno mwingine katika kiyunani linatumika neno “Allos” ambalo maana yake, The other, another, more one, yaani mwingine, tofauti na Yesu lakini akiwa katika kiwango kimoja au sawa na yeye kwa hiyo lugha hii pia inatufundisha kuwa huyu Msaidizi mwingine yaani Roho Mtakatifu ni nafsi tofauti na Yesu na ni nafsi nyingine tofauti na Baba lakini ni watenda kazi pamoja katika kukamilisha kusudi lile lile na hii inatuthibitishia kuwepo kwa utatu wa Mungu katika maana nyingine angalia maneno yale  Nami nitamwomba Baba, naye atawapa Msaidizi mwinginehii inathibitisha ukweli kuwa yuko Baba, Mwana na Roho Mtakatifu kwa hiyo mafundisho kuhusu utatu wa Mungu sio swala la kizushi lakini ni fundisho jepesi na rahisi la kimaandiko na bwana hajawahi kutukemea au kutufunulia kuwa hakuna usahihi katika hilo,

Mathayo 28:19-20 “Basi, enendeni, mkawafanye mataifa yote kuwa wanafunzi, mkiwabatiza kwa jina la Baba, na Mwana, na Roho Mtakatifu; na kuwafundisha kuyashika yote niliyowaamuru ninyi; na tazama, mimi nipo pamoja nanyi siku zote, hata ukamilifu wa dahari.”

Luka 3:21-22 “Ikawa, watu wote walipokwisha kubatizwa, na Yesu naye amebatizwa, naye anaomba, mbingu zilifunuka; Roho Mtakatifu akashuka juu yake kwa mfano wa kiwiliwili, kama hua; sauti ikatoka mbinguni, Wewe ndiwe Mwanangu, mpendwa wangu; nimependezwa nawe.”

Kwa hiyo msaidizi mwingine huyu ni nafsi nyingine mbali na baba na mwana Huyu ni Roho Mtakatifu, ukweli huu kuhusu namna Mungu alivyo katika utatu haupingiki kimaandiko kwa sababu neno la Mungu ndio linavyotuambia na kutuelekeza na kutufundisha, kwa hiyo Msaidizi mwingine ni Roho Mtakatifu, ni Roho wa Mungu, ni Mungu ndani yetu.                        

Umuhimu wa kuwa na Msaidizi mwingine

Ni muhimu kufahamu kuwa kuna umuhimu mkubwa sana wa kila mtu aliyeokolewa kuwa na uhusiano na Msaidizi mwingine yaani Roho Mtakatifu, Yesu alikuwa na maana pana sana ya kusisitiza kuwa atamuomba Baba ili atupatie Msaidizi mwingine yaani Roho Mtakatifu ili akae nasi, Yesu alikuwa anafahamu umuhimu wa Roho wa Mungu katika maisha yetu kwa sababu Yeye aliishi duniani kama Mwanadamu kwa asilimia 100% na akiwa Mungu kwa asilimia 100% Lakini kama mwanadamu alikuwa anataka kutufundisha namna ya kuishi na kutenda kama wana wa Mungu tukiwa hapa Duniani, alipokuwa Duniani Yesu alimtegemea Roho Mtakatifu kwa kila jambo kwa hiyo kila alichokifanya alikifanya kwa uwezo wa Roho Mtakatifu, Sasa ikiwa Bwana Yesu alimuhitaji Roho Mtakatifu katika maisha yake ni zaidi sana wewe na mimi tunamuhitaji zaidi.  Katika maisha yetu ili aweze kutusaidia katika kila jambo, Na ni muhimu kuelewa kuwa Roho Mtakatifu sio ushawishi, wala sio nguvu tu kama watu wengine wanavyofundisha bali ni Mungu kamili, Roho wa Mungu ni Mungu ona:-

Matendo 5:3-4 “Petro akasema, Anania, kwa nini Shetani amekujaza moyo wako kumwambia uongo Roho Mtakatifu, na kuzuia kwa siri sehemu ya thamani ya kiwanja?Kilipokuwa kwako, hakikuwa mali yako? Na kilipokuwa kimekwisha kuuzwa, thamani yake haikuwa katika uwezo wako? Ilikuwaje hata ukaweka neno hili moyoni mwako? Hukumwambia uongo mwanadamu, bali Mungu.”

Mathayo 12:22-28 “Wakati ule akaletewa mtu mwenye pepo, kipofu, naye ni bubu; akamponya, hata yule bubu akanena na kuona. Makutano wote wakashangaa, wakasema, Huyu siye mwana wa Daudi? Lakini Mafarisayo waliposikia, walisema, Huyu hatoi pepo, ila kwa Beelzebuli mkuu wa pepo. Basi Yesu akijua mawazo yao, akawaambia, Kila ufalme ukifitinika juu ya nafsi yake, hufanyika ukiwa; tena mji au nyumba yo yote ikifitinika juu ya nafsi yake, haitasimama. Na Shetani akimtoa Shetani, amefitinika juu ya nafsi yake; basi ufalme wake utasimamaje? Na mimi nikitoa pepo kwa Beelzebuli, je! Wana wenu huwatoa kwa nani? Kwa sababu hiyo hao ndio watakaowahukumu. Lakini mimi nikitoa pepo kwa Roho wa Mungu, basi ufalme wa Mungu umekwisha kuwajilia.”

Yesu Kristo alitoa kipaumbele kwa Roho Mtakatifu, alimtegemea Roho Mtakatifu hata kufanya miujiza na kutoa pepo, Nyakati za kanisa la kwanza walitoa kipaumbele kikubwa kwa Roho Mtakatifu, kwa msingi huo basi ni muhimu kwetu, kuhakikisha kuwa tunatoa nafasi kwa Roho Mtakatifu kwa sababu gani yeye anashughulika na maswala yote muhimu yanayohusiana na maisha yetu mfano:-

1.       Roho Mtakatifu huuisha Maisha mapya -  Roho Mtakatifu ndiye anayehusika kuweka mfumo wa maisha mapya katika roho zetu, ni yeye anayehusika katika wokovu wetu, na anakuwa kama anatuzaa upya kwa Roho, anatufufua kutoka katika hali ya kufa, anatupa uhai anatuhuuisha anaweka ndani yetu kiu ya kumcha Mungu na kumtafuta Mungu, hatuwezi kupata uamsho wowote ndani yetu ambao pia unaweza kuwa uamsho wa kanisa zima kama hatutamtii na kumsikiliza Roho Mtakatifu, mwanadamu anazaliwa akiwa ni mwenye dhambi kwa sababu ya kuifuata kawaida ya ulimwengu huu, Dhambi hutufarikisha na Mungu, mbele za Mungu mtu mwenye dhambi au aliyepotea huhesabiwa kama mfu, kwa sababu ametengwa mbali na uwepo wa Mungu

 

Waefeso 2:1-6 “Nanyi mlikuwa wafu kwa sababu ya makosa na dhambi zenu; ambazo mliziendea zamani kwa kuifuata kawaida ya ulimwengu huu, na kwa kumfuata mfalme wa uwezo wa anga, roho yule atendaye kazi sasa katika wana wa kuasi; ambao zamani, sisi sote nasi tulienenda kati yao, katika tamaa za miili yetu, tulipoyatimiza mapenzi ya mwili na ya nia, tukawa kwa tabia yetu watoto wa hasira kama na hao wengine. Lakini Mungu, kwa kuwa ni mwingi wa rehema, kwa mapenzi yake makuu aliyotupenda;hata wakati ule tulipokuwa wafu kwa sababu ya makosa yetu; alituhuisha pamoja na Kristo; yaani, tumeokolewa kwa neema. Akatufufua pamoja naye, akatuketisha pamoja naye katika ulimwengu wa roho, katika Kristo Yesu;”

 

Yohana 7:37-39 “Hata siku ya mwisho, siku ile kubwa ya sikukuu, Yesu akasimama, akapaza sauti yake akisema, Mtu akiona kiu, na aje kwangu anywe. Aniaminiye mimi, kama vile maandiko yalivyonena, mito ya maji yaliyo hai itatoka ndani yake. Na neno hilo alilisema katika habari ya Roho, ambaye wale wamwaminio watampokea baadaye; kwa maana Roho alikuwa hajaja, kwa sababu Yesu alikuwa hajatukuzwa.”

 

Uhai wote wa kimwili na wa kiroho uko katika uweza wa Roho Mtakatifu, bila Roho wa Mungu ni vigumu kitu chochote kuwa hai na maisha yetu ya kiroho kuwa hai, hatuwezi kuendelea, hatuwezi kujutia, hatuwezi kutubu, hatuwezi kuomba, hatuwezi kusoma neno la Mungu endapo Roho Mtakatifu hatahusika katika maisha yetu, kama ilivyo kwamba Bila Yesu hatuwezi kufanya neno lolote hali kadhalika Bila Roho wa Bwana sisi nasi hatuwezi kufanya jambo lolote, kwa hiyo Kristo alijua kuwa wanafunzi wake wamemuamini, lakini wasipokuwa na Roho Mtakatifu ni vigumu kwao kuendelea na imani ile bila ya msaada ulio karibu na msaada huo ni Roho Mtakatifu ambaye ndiye anayehuisha Roho zetu, Na kutupa msaada wa kuwa hai katika maswala ya kiroho.         

 

2.       Roho Mtakatifu hukaa ndani ya Mwamini – Kuna umuhimu mkubwa sana wa Roho Mtakatifu kukaa ndani yetu, Katika mstari wa Msingi tunamuona Yesu akisema atamuomba baba atupe msaidizi mwingine, ili msaidizi huyo akae ndani yetu

 

Yohana 14:16-18 “Nami nitamwomba Baba, naye atawapa Msaidizi mwingine, ili akae nanyi hata milele; ndiye Roho wa kweli; ambaye ulimwengu hauwezi kumpokea, kwa kuwa haumwoni wala haumtambui; bali ninyi mnamtambua, maana anakaa kwenu, naye atakuwa ndani yenu. Sitawaacha ninyi yatima; naja kwenu.”

 

Kukaa ndani yetu kwa Roho Mtakatifu kuna faida kubwa sana kwa sababu sisi ni hekalu la Roho Mtakatifu na akiwa ndani yetu tunapata nafasi ya kudumisha uhusiano wetu na Mungu kwa kuabudu, kuomba, kutafakari na kutuvuta tuwe karibu na yeye, Roho Mtakatifu anatumika kama daraja linalounganisha mioyo yetu na moyo wa Mungu, huku akibadilisha tabia zetu kwa kadiri tunavyojitoa kwake kwa kutii anatusababishia kuzaa matunda ya Roho na kuwa na sifa zinazomfanania Yesu Kristo.

 

Wagalatia 5:22-23 “Lakini tunda la Roho ni upendo, furaha, amani, uvumilivu, utu wema, fadhili, uaminifu, upole, kiasi; juu ya mambo kama hayo hakuna sheria.”

 

3.       Roho Mtakatifu hutupa hakika ya wokovu -  Tunapa hakika ya wokovu kwa Imani kupitia Roho wa Mungu ndani yetu, aidha na neno la Mungu kwa hiyo  wokovu wetu hautegemei hisia zetu namna tunavyojisikia lakini unategemea namna Neno la Mungu linavyotuambia tukithibitishiwa na Roho wake Mtakatifu

 

Warumi 8:15-16 “Kwa kuwa hamkupokea tena roho wa utumwa iletayo hofu; bali mlipokea roho ya kufanywa wana, ambayo kwa hiyo twalia, Aba, yaani, Baba. Roho mwenyewe hushuhudia pamoja na roho zetu, ya kuwa sisi tu watoto wa Mungu;”

 

4.       Roho Mtakatifu hubatiza mwamini – Neno la Mungu liliahidi ya kuwa sote tutabatizwa katika Roho Mtakatifu, Yohana mbatizaji anasema ajaye nyuma yangu ana nguvu kwa sababu yeye atawabatiza kwa Roho Mtakatifu, kwa hiyo ni kazi ya Mungu kutubatiza kwa Roho wake Mtakatifu, lugha inayofahamika kama kujazwa, kutujaza,  lugha nzuri ya maana sana ni ubatizo wa Roho Mtakatifu, na hata hivyo, anapotubatiza Roho mwenyewe huusika katika kutubatiza, tunazamishwa ndani yake na kila kitu mpaka lugha zetu zinaingizwa katika uwepo wa Roho Mtakatifu bila kutupagaa, “we are filled without possessed”

 

Mathayo 3:11 “Kweli mimi nawabatiza kwa maji kwa ajili ya toba; bali yeye ajaye nyuma yangu ana nguvu kuliko mimi, wala sistahili hata kuvichukua viatu vyake; yeye atawabatiza kwa Roho Mtakatifu na kwa moto.”

 

Yohana 1:33 “Wala mimi sikumjua; lakini yeye aliyenipeleka kubatiza kwa maji, huyo aliniambia, Yeye ambaye utamwona Roho akishuka na kukaa juu yake, huyo ndiye abatizaye kwa Roho Mtakatifu.”

 

Matendo 1:5 “ya kwamba Yohana alibatiza kwa maji, bali ninyi mtabatizwa katika Roho Mtakatifu baada ya siku hizi chache.”

 

Matendo 2:4 “Wote wakajazwa Roho Mtakatifu, wakaanza kusema kwa lugha nyingine, kama Roho alivyowajalia kutamka.”

               

Matendo 10:44-47 “Petro alipokuwa akisema maneno hayo Roho Mtakatifu akawashukia wote waliolisikia lile neno. Na wale waliotahiriwa, walioamini, wakashangaa, watu wote waliokuja pamoja na Petro, kwa sababu Mataifa nao wamemwagiwa kipawa cha Roho Mtakatifu.Kwa maana waliwasikia wakisema kwa lugha, na kumwadhimisha Mungu. Ndipo Petro akajibu, Ni nani awezaye kuzuia maji, hawa wasibatizwe, watu waliopokea Roho Mtakatifu vile vile kama sisi?

               

Matendo 19:1-6 “Ikawa, Apolo alipokuwa Korintho, Paulo, akiisha kupita kati ya nchi za juu, akafika Efeso; akakutana na wanafunzi kadha wa kadha huko; akawauliza, Je! Mlipokea Roho Mtakatifu mlipoamini? Wakamjibu, La, hata kusikia kwamba kuna Roho Mtakatifu hatukusikia. Akawauliza, Basi mlibatizwa kwa ubatizo gani? Wakasema, Kwa ubatizo wa Yohana. Paulo akasema, Yohana alibatiza kwa ubatizo wa toba, akiwaambia watu wamwamini yeye atakayekuja nyuma yake, yaani, Yesu. Waliposikia haya wakabatizwa kwa jina la Bwana Yesu. Na Paulo, alipokwisha kuweka mikono yake juu yao, Roho Mtakatifu akaja juu yao; wakaanza kunena kwa lugha, na kutabiri.”

               

Marko 16:17 “Na ishara hizi zitafuatana na hao waaminio; kwa jina langu watatoa pepo; watasema kwa lugha mpya;”

 

1Wakorintho 12:13 “Kwa maana katika Roho mmoja sisi sote tulibatizwa kuwa mwili mmoja, kwamba tu Wayahudi, au kwamba tu Wayunani; ikiwa tu watumwa au ikiwa tu huru; nasi sote tulinyweshwa Roho mmoja.”

 

1Wakorintho 14:2 “Maana yeye anenaye kwa lugha, hasemi na watu, bali husema na Mungu; maana hakuna asikiaye; lakini anena mambo ya siri katika roho yake.”

 

1Wakorintho 14:4 “Yeye anenaye kwa lugha hujijenga nafsi yake; bali ahutubuye hulijenga kanisa.”

 

5.       Roho Mtakatifu huzungumza na waamini – Roho Mtakatifu huzungumza, hunena na kuelekeza wazi wazi, ni jambo la kushangaza wale wanaodhani kuwa Roho Mtakatifu ni nguvu tu za Mungu na kumuondolea haki ya kuwa nafsi ni muhimu kujikumbusha kuwa huyu ni Msaidizi mwingine ni nafsi nyingine lakini anafanya kazi moja na Baba na Mwana na hivyo hutoa maelekezo, huzungumza, na hutoa maonyo.

 

Matendo 8:27-29 “Naye akaondoka, akaenda; mara akamwona mtu wa Kushi, towashi, mwenye mamlaka chini ya Kandake malkia wa Kushi, aliyewekwa juu ya hazina yake yote; naye alikuwa amekwenda Yerusalemu kuabudu, akawa akirejea, ameketi garini mwake akisoma chuo cha nabii Isaya. Roho akamwambia Filipo, Sogea karibu na gari hili, ukashikamane nalo.”

 

Matendo 13:1-2 “Na huko Antiokia katika kanisa lililokuwako palikuwa na manabii na waalimu, nao ni Barnaba, na Simeoni aitwaye Nigeri, na Lukio Mkirene, na Manaeni aliyekuwa ndugu wa kunyonya wa mfalme Herode, na Sauli.Basi hawa walipokuwa wakimfanyia Bwana ibada na kufunga, Roho Mtakatifu akasema, Nitengeeni Barnaba na Sauli kwa kazi ile niliyowaitia.”         

 

1Timotheo 4:1-3 “Basi Roho anena waziwazi ya kwamba nyakati za mwisho wengine watajitenga na imani, wakisikiliza roho zidanganyazo, na mafundisho ya mashetani; kwa unafiki wa watu wasemao uongo, wakichomwa moto dhamiri zao wenyewe; wakiwazuia watu wasioe, na kuwaamuru wajiepushe na vyakula, ambavyo Mungu aliviumba vipokewe kwa shukrani na walio na imani wenye kuijua hiyo kweli.”

               

Ufunuo 2:7 “Yeye aliye na sikio, na alisikie neno hili ambalo Roho ayaambia makanisa. Yeye ashindaye, nitampa kula matunda ya mti wa uzima, ulio katika bustani ya Mungu.”

               

Ufunuo 2:11Yeye aliye na sikio, na alisikie neno hili ambalo Roho ayaambia makanisa. Yeye ashindaye hatapatikana na madhara ya mauti ya pili.”        

 

Ufunuo 2:17Yeye aliye na sikio, na alisikie neno hili ambalo Roho ayaambia makanisa. Yeye ashindaye nitampa baadhi ya ile mana iliyofichwa, nami nitampa jiwe jeupe, na juu ya jiwe hilo limeandikwa jina jipya asilolijua mtu ila yeye anayelipokea.”               

 

Ufunuo 2:29 “Yeye aliye na sikio, na alisikie neno hili ambalo Roho ayaambia makanisa.”

 

6.       Roho Mtakatifu hujihusisha na uongozi wa kiroho – Wakati wanafunzi wakiwa Pamoja na Yesu Kristo Duniani yeye ndiye alikuwa kiongozi wao katika maswala yote ya kiroho na ibada, sasa Yesu anapokuwa Mbinguni huku akiwa pamoja nasi katika ulimwengu wa Roho, kila wajibu na kazi alizokuwa akizifanya sasa Roho Mtakatifu hufanya hivyo ndani yetu

 

Yohana 16:7 “Lakini mimi nawaambia iliyo kweli; yawafaa ninyi mimi niondoke, kwa maana mimi nisipoondoka, huyo Msaidizi hatakuja kwenu; bali mimi nikienda zangu, nitampeleka kwenu.”            

 

7.       Roho Mtakatifu hufundisha na Kuongoza katika kweli – Roho Mtakatifu ni Mwalimu mkuu, ambaye anapokuwa ndani yetu anatufundisha na kutukumbusha wote tuliomuamini katika neno la Kristo, jambo ambalo ni muhimu sana kwa ukuaji wetu kiroho na kudumu katika neno la Mungu na kuisimamia Imani, angalia leo wako watu wanaoukana utatu wazi wazi wakisema kuwa ni jambo lililoingizwa na Warumi wakati wa utawala wa Mfalme Constantino, wanasahahu kuwa mfalme huyo aliokoka baada ya kuona alama ya msalaba mbinguni wakati wa usiku na sauti iliyomuambia kuwa kwa alama hii utashinda na ndipo alipoukubali Ukristo, Mungu alimtumia kusimamia kweli kadhaa pamoja na wazee wetu kwa uwezo wa Roho Mtakatifu, ni kweli kuwa kanisa katoliki lina madhaifu kadhaa kama yalivyo makanisa mengine na kama yalivyokuwa yale makanisa saba ya eneo la Asia ndogo ambayo Yesu aliyakemea mapungufu yao na kuwatia moyo uwezo wao, hata hivyo pamoja na udhaifu unaoweza kuuona kwa wakatoliki hawajawahi kufikia ngazi ya kukana uungu wa Yesu au uungu wa Roho Mtakatifu, kwa hiyo katika wakati huu wa kuishi  kwetu tunapaswa kumtegemea sana Roho Mtakatifu kutuongoza katika kweli badala ya kushiba maharagwe na kuropoka, maandiko yako wazi kuhusu utatu wa Mungu likiwemo hili ya kuwa Roho Mtakatifu ni Mwalimu kama vile vile ilivyokuwa kwa Yesu Kristo, na atatukumbusha  na kutuongoza na kututia katika kweli yote.  

 

Yohana 14:26 “Lakini huyo Msaidizi, huyo Roho Mtakatifu, ambaye Baba atampeleka kwa jina langu, atawafundisha yote, na kuwakumbusha yote niliyowaambia.”

 

Yohana 16:13-15 “Lakini yeye atakapokuja, huyo Roho wa kweli, atawaongoza awatie kwenye kweli yote; kwa maana hatanena kwa shauri Lake Mwenyewe, lakini yote atakayoyasikia atayanena, na mambo yajayo atawapasha habari yake. Yeye atanitukuza mimi, kwa kuwa atatwaa katika yaliyo yangu na kuwapasha habari. Na yote aliyo nayo Baba ni yangu; kwa hiyo nalisema ya kwamba atatwaa katika yaliyo yangu, na kuwapasheni habari

 

8.       Roho Mtakatifu huita watu katika huduma – Roho Mtakatifu huita watu katika huduma na kuwaongoza katika huduma hiyo sawasawa na Yesu alivyokuwa akiita watu na wote wanaongoza katika kazi ileile kwa misingi ile ile, mfano unaweza kumuona Yesu akimuita Sauli kwa kazi yake na unaweza kumuona Roho wa Mungu akimuita sauli yule yule aliyeitwa na Yesu kwa kazi ile iole iliyokusudiwa na Bwan Yesu! Ona :-

 

Matendo 9:1-6 “Lakini Sauli, akizidi kutisha na kuwaza kuwaua wanafunzi wa Bwana, akamwendea Kuhani Mkuu,akataka ampe barua za kuenda Dameski zilizoandikwa kwa masinagogi, ili akiona watu wa Njia hii, waume kwa wake, awafunge na kuwaleta Yerusalemu.Hata alipokuwa akisafiri, ikawa anakaribia Dameski; ghafula ikamwangaza kote kote nuru kutoka mbinguni. Akaanguka chini, akasikia sauti ikimwambia, Sauli, Sauli, mbona waniudhi?Akasema, U nani wewe, Bwana? Naye akasema, Mimi ndimi Yesu unayeniudhi wewe. Lakini simama, uingie mjini, nawe utaambiwa yakupasayo kutenda.”

 

Matendo 13:1-4 “Na huko Antiokia katika kanisa lililokuwako palikuwa na manabii na waalimu, nao ni Barnaba, na Simeoni aitwaye Nigeri, na Lukio Mkirene, na Manaeni aliyekuwa ndugu wa kunyonya wa mfalme Herode, na Sauli. Basi hawa walipokuwa wakimfanyia Bwana ibada na kufunga, Roho Mtakatifu akasema, Nitengeeni Barnaba na Sauli kwa kazi ile niliyowaitia. Ndipo wakiisha kufunga na kuomba, wakaweka mikono yao juu yao, wakawaacha waende zao Basi watu hao, wakiisha kupelekwa na Roho Mtakatifu wakatelemkia Seleukia, na kutoka huko wakasafiri baharini hata Kipro.”    

 

Matendo 16:6-10 “Wakapita katika nchi ya Frigia na Galatia, wakikatazwa na Roho Mtakatifu, wasilihubiri lile neno katika Asia. Walipofika kukabili Misia wakajaribu kuenda Bithinia, lakini Roho wa Yesu hakuwapa ruhusa, wakapita Misia wakatelemkia Troa. Paulo akatokewa na maono usiku; alimwona mtu wa Makedonia amesimama, akimsihi, na kumwambia, Vuka, uje Makedonia utusaidie. Basi alipokwisha kuyaona yale maono, mara tukataka kutoka kwenda Makedonia, kwa kuwa tuliona hakika ya kwamba Mungu ametuita tuwahubiri Habari Njema.”

 

9.       Roho Mtakatifu hutupa uhakika wa uwepo wa Mungu – Roho Mtakatifu anakaa ndani yetu na anafanya kazi ya kutupa uhakika wa uwepo wa Mungu na uwepo halisi wa Yesu Kristo na asili zao na zaidi ya yote anatuunga katika ushirika na Mungu Baba na Mwana  na ndio maana maandiko yana wasiwasi sana na mtu ambaye anaharibu asili ya Mungu baba na Mungu mwana na wakati mwingine watu wanaofanya hivyo huenda hawana Roho wa Mungu ndani yao kama maandiko yanavyotuonya wazi wazi

 

1Yohana 2:22-29 “Ni nani aliye mwongo ila yeye akanaye ya kuwa Yesu ni Kristo? Huyo ndiye mpinga Kristo, yeye amkanaye Baba na Mwana.Kila amkanaye Mwana, hanaye Baba; amkiriye Mwana anaye Baba pia.Ninyi basi, hilo mlilolisikia tangu mwanzo na likae ndani yenu. Ikiwa hilo mlilolisikia tangu mwanzo linakaa ndani yenu, ninyi nanyi mtakaa ndani ya Mwana, na ndani ya Baba. Na hii ndiyo ahadi aliyotuahidia, yaani, uzima wa milele. Nimewaandikia haya katika habari za watu wale wanaotaka kuwapoteza. Nanyi, mafuta yale mliyoyapata kwake yanakaa ndani yenu, wala hamna haja ya mtu kuwafundisha; lakini kama mafuta yake yanavyowafundisha habari za mambo yote, tena ni kweli wala si uongo, na kama yalivyowafundisha, kaeni ndani yake. Na sasa, watoto wadogo, kaeni ndani yake, ili kusudi, atakapofunuliwa, mwe na ujasiri, wala msiaibike mbele zake katika kuja kwake.Kama mkijua ya kuwa yeye ni mwenye haki, jueni ya kuwa kila atendaye haki amezaliwa na yeye.”

 

Warumi 8:9-16 “Lakini ikiwa Roho wa Mungu anakaa ndani yenu, ninyi hamwufuati mwili; bali mwaifuata roho. Lakini mtu awaye yote asipokuwa na Roho wa Kristo, huyo si wake. Na Kristo akiwa ndani yenu, mwili wenu umekufa kwa sababu ya dhambi; bali roho yenu i hai, kwa sababu ya haki. Lakini, ikiwa Roho yake yeye aliyemfufua Yesu katika wafu anakaa ndani yenu, yeye aliyemfufua Kristo Yesu katika wafu ataihuisha na miili yenu iliyo katika hali ya kufa, kwa Roho wake anayekaa ndani yenu. Basi, kama ni hivyo, ndugu, tu wadeni, si wa mwili tuishi kwa kufuata mambo ya mwili, kwa maana kama tukiishi kwa kufuata mambo ya mwili, mwataka kufa; bali kama mkiyafisha matendo ya mwili kwa Roho, mtaishi. Kwa kuwa wote wanaoongozwa na Roho wa Mungu, hao ndio wana wa Mungu. Kwa kuwa hamkupokea tena roho wa utumwa iletayo hofu; bali mlipokea roho ya kufanywa wana, ambayo kwa hiyo twalia, Aba, yaani, Baba. Roho mwenyewe hushuhudia pamoja na roho zetu, ya kuwa sisi tu watoto wa Mungu;”

 

10.   Roho Mtakatifu hutia nguvu – Roho wa Mungu hututia nguvu kukamilisha majukumu yote tuliyopewa na Mungu hapa duniani hasa ya kuhudumia watu, pamoja na kukabiliana na nguvu zote pinzani zinazotukabili kwa kusudi la kuzuia kusudi la Mungu, na kutimiza majukumu yote ambayo Mungu anataka tuwatendee watu wake

 

Luka 4:18-19 “Roho wa Bwana yu juu yangu, Kwa maana amenitia mafuta kuwahubiri maskini habari njema. Amenituma kuwatangazia wafungwa kufunguliwa kwao, Na vipofu kupata kuona tena, Kuwaacha huru waliosetwa,Na kutangaza mwaka wa Bwana uliokubaliwa.”

 

Matendo 1:8 “Lakini mtapokea nguvu, akiisha kuwajilia juu yenu Roho Mtakatifu; nanyi mtakuwa mashahidi wangu katika Yerusalemu, na katika Uyahudi wote, na Samaria, na hata mwisho wa nchi.”

 

11.   Roho Mtakatifu husaidia katika maombi – Tangu zamani uwezo wa kuomba hauko katika uweza wa wanadamu, Roho Mtakatifu ndiye anayetuwezesha kuomba kwa kuugua kusikoweza kutamkwa au kwa kuomboleza, waamini wanapoomba pamoja na Roho Mtakatifu hawachoki, na sio hivyo tu huomba katika namna iliyo sahihi, Yeye anaitwa Roho wa neema na kuomba maana yake hutusaidia au kutupa neema ya kuomba, Maisha ya mtu aliyeokoka yatapata usitawi mkubwa sana endapo watu wake wataomba wakisaidiwa na Roho Mtakatifu.

 

Zekaria 12:10 “Nami nitawamwagia watu wa nyumba ya Daudi, na wenyeji wa Yerusalemu, roho ya neema na kuomba; nao watamtazama yeye ambaye walimchoma; nao watamwombolezea, kama vile mtu amwombolezeavyo mwanawe wa pekee; nao wataona uchungu kwa ajili yake, kama vile mtu aonavyo uchungu kwa ajili ya mzaliwa wake wa kwanza.”

 

Warumi 8:26-28 “Kadhalika Roho naye hutusaidia udhaifu wetu, kwa maana hatujui kuomba jinsi itupasavyo, lakini Roho mwenyewe hutuombea kwa kuugua kusikoweza kutamkwa.Na yeye aichunguzaye mioyo aijua nia ya Roho ilivyo, kwa kuwa huwaombea watakatifu kama apendavyo Mungu.Nasi twajua ya kuwa katika mambo yote Mungu hufanya kazi pamoja na wale wampendao katika kuwapatia mema, yaani, wale walioitwa kwa kusudi lake.”

 

Yuda 1:20 “Bali ninyi, wapenzi, mkijijenga juu ya imani yenu iliyo takatifu sana, na kuomba katika Roho Mtakatifu,”                       

 

12.   Roho Mtakatifu huwezesha kuabudu – Mungu ni Roho nao waabuduo halisi wanapaswa kumuabudu yeye katika Roho na kweli, kimsingi hatuwezi kuabudu vizuri bila msaada wa Roho Mtakatifu kama tu vile jinsi ambavyo hatuwezi kuomba vizuri bila Roho Mtakatifu, muunganiko wetu na usikivu wetu katika kumuabudu Mungu na kupokea kutoka kwake unatuhitaji wakati wa kuabudu tuwe rohoni

 

Ufunuo 1:9-11 “Mimi Yohana, ndugu yenu na mwenye kushiriki pamoja nanyi katika mateso na ufalme na subira ya Yesu Kristo, nalikuwa katika kisiwa kiitwacho Patmo, kwa ajili ya Neno la Mungu, na ushuhuda wa Yesu. Nalikuwa katika Roho, siku ya Bwana; nikasikia sauti kuu nyuma yangu, kama sauti ya baragumu,ikisema, Haya uyaonayo uyaandike katika chuo, ukayapeleke kwa hayo makanisa saba: Efeso, na Smirna, na Pergamo, na Thiatira, na Sardi, na Filadelfia, na Laodikia.”

 

Yohana 4:23-24 “Lakini saa inakuja, nayo sasa ipo, ambayo waabuduo halisi watamwabudu Baba katika roho na kweli. Kwa maana Baba awatafuta watu kama hao wamwabudu.Mungu ni Roho, nao wamwabuduo yeye imewapasa kumwabudu katika roho na kweli.”

               

Wafilipi 3:3 “Maana sisi tu tohara, tumwabuduo Mungu kwa Roho, na kuona fahari juu ya Kristo Yesu, wala hatuutumainii mwili.”

 

1Wakorintho 14:15 “Imekuwaje, basi? Nitaomba kwa roho, tena nitaomba kwa akili pia; mtaimba kwa roho, tena nitaimba kwa akili pia.”               

 

13.   Roho Mtakatifu hutoa karama – Kwaajili ya kuifanikisha kazi ya Mungu Roho wa Mungu hutupa karama ambazo kazi yake ni kuujenga mwili wa Kristo na kulithibitisha neno la Mungu, miujiza yote, uponyaji utoaji wa pepo ni kazi zinazofanywa na Roho Mtakatifu kupitia karama mbalimbalia anazoziweka kwa waamini

 

1Wakorintho 12:7-11 “Lakini kila mmoja hupewa ufunuo wa Roho kwa kufaidiana. Maana mtu mmoja kwa Roho apewa neno la hekima; na mwingine neno la maarifa, apendavyo Roho yeye yule; mwingine imani katika Roho yeye yule; na mwingine karama za kuponya katika Roho yule mmoja; na mwingine matendo ya miujiza; na mwingine unabii; na mwingine kupambanua roho; mwingine aina za lugha; na mwingine tafsiri za lugha; lakini kazi hizi zote huzitenda Roho huyo mmoja, yeye yule, akimgawia kila mtu peke yake kama apendavyo yeye.”

               

Kuna na mambo mengine mengi sana ambayo msaidizi mwingine huyafanya katika maisha yetu ya kila siku, hapa nimechagua machache lakini ni msaada kwa wanafunzi wakati wa mitihani, ni msaada kwa wanajeshi wakiwa vitani, ni msaada kwa usalama wa taifa na wapelelezi,  ni msaada wa wafalme katika maamuzi, ni msaada kwa wafanya biashara, ni msaada kwa wakulima, ni msaada kwa wachumi na ni msaada katika michezo na kila eneo ambalo Mtu wa Mungu analifanyia kazi, ni msaada kwa mafundi wa cherahani na wajenzi alitoa hekima kwa ujenzi wa hekalu, mavazi ya Haruni, wajenzi wa hema, ujenzi wa Meli wakati wa Nuhu, ukulima wakati wa Isaka, utawala wakati wa Suleimani, vitani wakati wa wamaamuzi na Daudi, upelelezi wakati wa Elisha,  kimsingi Roho wa Mungu ni msaada katika maisha yetu hata kitu kinapopotea Roho Mtakatifu, anahusika kionekane kumbuka habari ya kuelea kwa chuma cha shoka wakati wa Elisha na matukio mengine chungu nzima muimbaji na wapigaji kinubi kama Daudi mpaka pepo wanakimbia, vitani ngao zilipakwa mafuta kupata neema na upako kwaajili ya ushindi na ulinzi, unaweza kuhitaji msaada wa Roho Mtakatifu katika kila eneo bila kumuwekea Mungu mipaka.  Na ni kazi yake kutupa msaada tunaoutaka

Jinsi ya kuwa na msaidizi mwingine.

Roho Mtakatifu ili umpokee ni lazima uwe umemuamini Bwana Yesu kama mwokozi wako aliyekufa msalabani kwaajili yako, tendo la kumuamini Bwana Yesu ndilo linalotuunganisha na Mungu na kutufanya tuwe wana wa Mungu na kwa imani tunajiweka katika nafasi ya kumpokea Roho Mtakatifu

Matendo 2:38 “Petro akawaambia, Tubuni mkabatizwe kila mmoja kwa jina lake Yesu Kristo, mpate ondoleo la dhambi zenu, nanyi mtapokea kipawa cha Roho Mtakatifu.”     

Matendo 19:1-6 “Ikawa, Apolo alipokuwa Korintho, Paulo, akiisha kupita kati ya nchi za juu, akafika Efeso; akakutana na wanafunzi kadha wa kadha huko; akawauliza, Je! Mlipokea Roho Mtakatifu mlipoamini? Wakamjibu, La, hata kusikia kwamba kuna Roho Mtakatifu hatukusikia. Akawauliza, Basi mlibatizwa kwa ubatizo gani? Wakasema, Kwa ubatizo wa Yohana. Paulo akasema, Yohana alibatiza kwa ubatizo wa toba, akiwaambia watu wamwamini yeye atakayekuja nyuma yake, yaani, Yesu. Waliposikia haya wakabatizwa kwa jina la Bwana Yesu. Na Paulo, alipokwisha kuweka mikono yake juu yao, Roho Mtakatifu akaja juu yao; wakaanza kunena kwa lugha, na kutabiri.”

Yohana 7:38-39 “Aniaminiye mimi, kama vile maandiko yalivyonena, mito ya maji yaliyo hai itatoka ndani yake.Na neno hilo alilisema katika habari ya Roho, ambaye wale wamwaminio watampokea baadaye; kwa maana Roho alikuwa hajaja, kwa sababu Yesu alikuwa hajatukuzwa.”

Ni lazima mtu anayemuhitaji Roho Mtakatidu awe na shauku, liwe ni hitaji, iwe ni kiu yako na hivyo hua budi kuwa muhitaji na kumuomba Mungu baada ya kujifunza umuhimu wake unaingia katika maombi unaomba na Mungu anapoiona shauku yako na kiu yako atakupa Roho Mtakatifu.

Luka 11:13 “Basi, ikiwa ninyi mlio waovu mnajua kuwapa watoto wenu vipawa vyema, je! Baba aliye mbinguni hatazidi sana kuwapa Roho Mtakatifu hao wamwombao?

Yohana 7:37-39 “Hata siku ya mwisho, siku ile kubwa ya sikukuu, Yesu akasimama, akapaza sauti yake akisema, Mtu akiona kiu, na aje kwangu anywe. Aniaminiye mimi, kama vile maandiko yalivyonena, mito ya maji yaliyo hai itatoka ndani yake.Na neno hilo alilisema katika habari ya Roho, ambaye wale wamwaminio watampokea baadaye; kwa maana Roho alikuwa hajaja, kwa sababu Yesu alikuwa hajatukuzwa.”

Ni lazima ukae katika neno la Mungu, Roho Mtakatifu hafanyi kazi nje ya neno lake lililowekwa ndani yetu kwa hiyo hakikisha unajaa neno na kwa jinsi hii utaruhusu Roho Mtakatifu kufanya makazi ndani yako na utaiona na kufurahia faida zake zote katika maisha yako

Yohana 15:7-8 “Ninyi mkikaa ndani yangu, na maneno yangu yakikaa ndani yenu, ombeni mtakalo lote nanyi mtatendewa. Hivyo hutukuzwa Baba yangu, kwa vile mzaavyo sana; nanyi mtakuwa wanafunzi wangu.”

Utii kwa neno la Mungu husafisha njia ya Roho Mtakatifi kukaa ndani yetu Zaburi 51:4-11“Nimekutenda dhambi Wewe peke yako, Na kufanya maovu mbele za macho yako. Wewe ujulikane kuwa una haki unenapo, Na kuwa safi utoapo hukumu.Tazama, mimi naliumbwa katika hali ya uovu; Mama yangu alinichukua mimba hatiani. Tazama, wapendezwa na kweli iliyo moyoni; Nawe utanijulisha hekima kwa siri, Unisafishe kwa hisopo nami nitakuwa safi, Unioshe, nami nitakuwa mweupe kuliko theluji Unifanye kusikia furaha na shangwe, Mifupa uliyoiponda ifurahi. Usitiri uso wako usitazame dhambi zangu; Uzifute hatia zangu zote. Ee Mungu, uniumbie moyo safi, Uifanye upya roho iliyotulia ndani yanguUsinitenge na uso wako, Wala roho yako mtakatifu usiniondolee.”

Jihadhari usiasi Isaya 63:10 “Lakini wakaasi, wakamhuzunisha Roho yake Mtakatifu; kwa hiyo akawageukia, akawa adui, akapigana nao.”

Kwa kuwa msaidizi mwingine ni wa Muhimu na ni zawadi kubwa sana kutoka kwa Mungu wakristo ni lazima tukubali kuruhusu Mungu atende kazi pamoja nasi kupitia Roho wake Mtakatifu kwaajili ya utukufu wake, hatuwezi lolote katika maisha haya na bila Mungu hatuwezi kutoboa kwa sababu hiyo ni muhimu kwetu kuhakikisha kuwa wakati wote tunampa Roho Mtakatifu kipaumbele katika maisha yetu na tunamtii kwa kila mzigo anaouweka ndani yetu na tuutimize kwa wakati. Uongezewe neema

Na Rev. Innocent Samuel Kamote

Mkuu wa wajenzi mwenye hekima