Jumatatu, 5 Februari 2018

Kama Mungu angekuwa Baba yako!



Yohana 8: 42Yesu akawaambia, Kama Mungu angekuwa baba yenu, mngenipenda mimi; kwa maana nalitoka kwa Mungu, nami nimekuja; wala sikuja kwa nafsi yangu, bali yeye ndiye aliyenituma.”


Utangulizi

Ni muhimu kwa kila mmoja wetu kujiuliza je Mungu ni baba yetu? Ni muhimu kufahamu kuwa sio kila mmoja wetu Mungu ni baba yake?, Yesu aliwahi kuwaambia ukweli mafarisayo na masadukayo pamoja na waalimu wa Torati waliodhani kuwa Mungu ni Baba yao kwamba wao sio wa Mungu, na aliwakemea kwa kuwaeleza wazi kuwa wao baba yao ni Ibilisi Yohana 8:44Ninyi ni wa baba yenu, Ibilisi, na tamaa za baba yenu ndizo mpendazo kuzitenda. Yeye alikuwa mwuaji tangu mwanzo; wala hakusimama katika kweli, kwa kuwa hamna hiyo kweli ndani yake. Asemapo uongo, husema yaliyo yake mwenyewe; kwa sababu yeye ni mwongo, na baba wa huo.” Kama Mungu ni baba yetu tutampenda Yesu, tutamkubali Yesu, na tunaweza kuthibitisha kwamba sisi ni wa baba katika njia kuu saba zifuatazo:-

1.       Tutamwanimi yeye kama tunavyomwamini Mungu:-

Ni jambo la kusikitisha kwamba Yesu alitoka kwa Mungu, lakini hata hivyo wakuu wa dini, mafarisayo na masadukayo pamoja na waandishi yaani walimu wa torati hawakuwa wamemwamini, huwezi kusema kuwa unampenda mtu, lakini hata hivyo humuamini, kuamini kunaendana na kupenda Yesu anataka tumwamini yeye kwa kiwango kilekile cha kumuamini Mungu Yohana 14:1Msifadhaike mioyoni mwenu; mnamwamini Mungu, niaminini na mimi.”

Ishara kubwa ya kwamba tunamkubali Yesu na kwamba tunamwamini Mungu na tunampenda ni pamoja na kumuamini, na kama tunamwamini Yesu ni sawa na kuwa tumekubali zawadi kubwa ambayo Mungu amewapa wanadamu kupitia yeye na hivyo tutampenda.

2.       Tutazitii amri zake:-

Kiwango kikubwa na cha juu zaidi cha upendo wetu kwa Yesu ni pamoja na kutii amri zake, Yesu aliliweka wazi hili mapema tu ya kwamba kama Mungu ni baba yetu na amemtuma mwanaye wa pekee sio tu ili tumwamini lakini vilevile tumsikilize yeye ni ukweli ulio wazi kuwa Torati iliagiza kuwa Nabii huyu mkubwa aliyetumwa kwa mfano wa Musa anapaswa kusikilizwa maana yake tumtii Kumbukumbu la Torati 18:15,18-19Bwana, Mungu wako, atakuondokeshea nabii miongoni mwa ndugu zako kama nilivyo mimi; msikilizeni yeye., Mimi nitawaondokeshea nabii miongoni mwa ndugu zao mfano wako wewe, nami nitatia maneno yangu kinywani mwake, naye atawaambia yote nitakayomwamuru.Hata itakuwa, mtu asiyesikiliza maneno yangu atakayosema yule kwa jina langu, nitalitaka kwake” Yesu alikuwa ndiye nabii yule ajaye aliyetabiriwa na Musa katika torati na katika manabii na swala hili lilieleweka wazi Yohana 1:45. “Filipo akamwona Nathanaeli, akamwambia, Tumemwona yeye aliyeandikiwa na Musa katika torati, na manabii, Yesu, mwana wa Yusufu, mtu wa Nazareti” ni ukweli ulio wazi kuwa ilieleweka kwamba Yesu ndiye masihi lakini hata hivyo baadhi ya watu licha ya kuwa walikataa kumuamini lakini pia hawakuzishika amri zake, Yesu anaweka wazi kuwa kama tunampenda yeye basi tutazitii amri zake Yohana 14:15Mkinipenda, mtazishika amri zangu” Unaona kama Mungu ni baba yetu tutamwanini Yesu Kristo na tutazishika mari zake.Yesu hafurahii kuitwa Bwana na watu ambao hawako tayari kuyatenda asemayo Luka 6:46Na kwa nini mnaniita, Bwana, Bwana, walakini hamyatendi nisemayo?” unaona Yesu kristo anahitaji kuaminiwa lakini vilevile kuyatii maagizo yake.

3.       Tutadumisha Ushirika wetu na Yesu!

Ni muhimu kufahamu kuwa uhusiano wetu na Mungu na bwana wetu Yesu Kristo ni uhusiano wa kudumu, awaye yote ambaye atamwamini Yesu au aliyeamua kumfuata Yesu hana budi kuhakikisha kuwa anashikamana na ushirika na Yesu bila kugeuka nyuma, Mungu anatarajia uhusiano wetu nay eye uwe wenye kudumu, na hafurahii kugeuka nyuma, kimsingi mtu anayemuacha Mungu biblia inamuita mtu mwenye moyo mbovu Waebrania 3:12-14 “Angalieni, ndugu zangu, usiwe katika mmoja wenu moyo mbovu wa kutokuamini, kwa kujitenga na Mungu aliye hai. Lakini mwonyane kila siku, maadamu iitwapo leo; ili mmoja wenu asifanywe mgumu kwa udanganyifu wa dhambi.  Kwa maana tumekuwa washirika wa Kristo, kama tukishikamana na mwanzo wa uthabiti wetu kwa nguvu mpaka mwisho;” Kuanza safari ya kumuamini Yesu sio tatizo, watu wengi hulipokea neno kwa furaha na kumkubali Bwana yesu kwa msisimko, lakini hata hivyo kuendelea kukaa ndani yake ndio jambo la muhimu na zaidi ya umuhimu ni kustahimili mpaka mwisho na kuumaliza mwendo pamoja naye, Mathayo 24:13Lakini mwenye kuvumilia hata mwisho, ndiye atakayeokoka.”  Unaweza kuona kwamba mtu anamalizaje hilo ndio jambo la muhimu, Katika kutuongoza kuifuata imani Biblia inatutia moyo kuwaiga watu waliotuongoza na kuiiga imani yao Waebrania 13:7 “Wakumbukeni wale waliokuwa wakiwaongoza, waliowaambia neno la Mungu; tena, kwa kuuchunguza sana mwisho wa mwenendo wao, iigeni imani yao.” Kumbe tunaweza kuiiga imani ya kiongozi wetu, wachungaji wetu, mashemasi wetu wazee wetu, maaskofu wetu na kadhalika lakini baada ya kuchunguza namna walivyohitimu katika imani, Mungu anataka tudumishe uhusiano nay eye hata mwisho.

4.       Tutazinena habari zake!

Hakuna namna yoyote ambayo kwayo tunaweza kusema kuwa tunampenda Mungu na Yesu Kristo kama hatuzisemi habari zake, Mitume walidhihirisha wazi kuwa wanampenda sio kwa kunyamaza kimya bali walizinena habari zake  kila siku na kila mahali Matendo 5:41-42Nao wakatoka katika ile baraza, wakifurahi kwa sababu wamehesabiwa kuwa wamestahili kuaibishwa kwa ajili ya Jina hilo.  Na kila siku, ndani ya hekalu na nyumbani mwao, hawakuacha kufundisha na kuhubiri habari njema za Yesu kwamba ni Kristo.Maandiko yanawasifia watu wanaonena habari za Yesu kuwa ni watu wema na kuisifia miguu yao kuwa ni mizuri, Yesu anataka tusambaze habari zake kwa watu wote ili waliitie jina lake na kuokolewa Warumi 10:14-15 “Basi wamwiteje yeye wasiyemwamini? Tena wamwaminije yeye wasiyemsikia? Tena wamsikieje pasipo mhubiri? Tena wahubirije, wasipopelekwa? Kama ilivyoandikwa, Ni mizuri kama nini miguu yao wahubirio habari ya mema!Nyakati za kanisa la kwanza watu walimpenda sana Yesu na hivyo hawakuacha kuzungumza habari zake kila walikokwenda hata pale walipotawanyika kwa sababu ya dhiki bado walikuwa waaminifu kuelezea habari za Yesu Matendo 8:1-5 “Siku ile kukatukia adha kuu ya kanisa lililokuwa katika Yerusalemu; wote wakatawanyika katika nchi ya Uyahudi na Samaria, isipokuwa hao mitume.  Watu watauwa wakamzika Stefano, wakamfanyia maombolezo makuu. Sauli akaliharibu kanisa, akiingia kila nyumba, na kuwaburuta wanaume na wanawake na kuwatupa gerezani. Lakini wale waliotawanyika wakaenda huko na huko wakilihubiri neno. Filipo akatelemka akaingia mji wa Samaria, akawahubiri Kristo.”  Kama Mungu ni baba yaetu tutampenda Yesu Kristo na kama tunampenda Yeu Kristo tutazungumza habari zake, Biblia inatutaka tuwe tayari wakati wote na siku zote 1Petro 3:15Mwe tayari siku zote kumjibu kila mtu awaulizaye habari za tumaini lililo ndani yenu; lakini kwa upole na kwa hofu.” Wote waliompenda Yesu walikuwa tayari kuzishuhudia habari zake na hawakuona aibu.

5.       Tutakuwa tayari kuteseka kwaajili yake

Kile unachokipenda wakati mwingine unaweza kuwa tayari kukigharimikia, wazazi wanatoa nguvu zao na muda wao kujinyima kwaajli ya watoto wao kwa vile wanawapenda, wako watu ambao wako tayari kuyatoa maisha yao kwaajili ya wapendwa wao, katika hali kama hii wote wanaompenda Yesu wote ambao Mungu ni aba yao watakuwa tayari pia kuteseka kwaajili ya Yesu Kristo , Yeye alitupatia zawadi kuu ya wokovu kwa njia ya Mateso Waebrania 5:7-9 7. “Yeye, siku hizo za mwili wake, alimtolea yule, awezaye kumwokoa na kumtoa katika mauti, maombi na dua pamoja na kulia sana na machozi, akasikilizwa kwa jinsi alivyokuwa mcha Mungu; na, ingawa ni Mwana, alijifunza kutii kwa mateso hayo yaliyompata; naye alipokwisha kukamilishwa, akawa sababu ya wokovu wa milele kwa watu wote wanaomtii;unaweza kuona jinsi ambayo kiongozi mkuu wa wokovu wetu yaani Bwana Yesu alikamilishwa kwa njia ya Mateso, kila mmoja wetu ambaye ameitwa kumwandama Bwana ni lazima pia awe tayari kuteseka kwaajili yake kuwa ndani ya Yesu ni kukubali mateso ni kujiunga  na mateso yake 2Timotheo 1:7-12 “7. Maana Mungu hakutupa roho ya woga, bali ya nguvu na ya upendo na ya moyo wa kiasi. Basi usiuonee haya ushuhuda wa Bwana wetu, wala usinionee haya mimi mfungwa wake, bali uvumilie mabaya pamoja nami kwa ajili ya Injili, kwa kadiri ya nguvu ya Mungu; ambaye alituokoa akatuita kwa mwito mtakatifu, si kwa kadiri ya matendo yetu sisi, bali kwa kadiri ya makusudi yake yeye na neema yake. Neema hiyo tulipewa katika Kristo Yesu tangu milele, na sasa inadhihirishwa kwa kufunuliwa kwake Mwokozi wetu Kristo Yesu; aliyebatili mauti, na kuufunua uzima na kutokuharibika, kwa ile Injili; ambayo kwa ajili ya hiyo naliwekwa niwe mhubiri na mtume na mwalimu. Kwa sababu hiyo nimepatikana na mateso haya, wala sitahayari; kwa maana namjua yeye niliyemwamini, na kusadiki ya kwamba aweza kukilinda kile nilichokiweka amana kwake hata siku ile.” Unaweza kuona njia nyingine pekee yenye kuonyesha kuwa tunampenda Mungu na kwamba Mungu ni baba yetu ni kukubali kushiriki mateso kwaajili ya injili yake.

6.       Tutatamani kufanana naye.  
     
Lengo kubwa la neno la Mungu na mafundisho ya mitume ni sisi kuwa kama Yesu Kristo Wagalatia 4:19Vitoto vyangu, ambao kwamba nawaonea utungu tena mpaka Kristo aumbike ndani yenu;” Unaona Kristo kuumbika ndani yetu maana yake ni ile hali ya kukomaa na katika tabia na mwenendo na kufikia hatua ya kuwa kama Yesu Kristo mwenyewe, hili ndilo kusudi kuu kama tunampenda Yesu ni lazima tutafanana naye, mwelekeo na mkazo mkuu wa mitume na manabii ni kuhakikisha kuwa tunawafuata wao kama wanavyomfuata Kristo 1Wakoritho 11:1Mnifuate mimi kama mimi ninavyomfuata Kristo.” Watoto wakati wote hujifunza kwa kuigiza tunaweza kuwaigiza wazazi wetu katika kila jambo liwe jema au baya, kwa sababu tunawapenda, sisi nasi kama tunampenda Bwana Yesu tutamuiga katika kila eneo la tabia na mwenendo wake, kuitwa wakristo kunatokana na mwenendo unaomfanania Yesu Kristo, Wakolosai 3:9-11Msiambiane uongo, kwa kuwa mmevua kabisa utu wa kale, pamoja na matendo yake;           mkivaa utu mpya, unaofanywa upya upate ufahamu sawasawa na mfano wake yeye aliyeuumba. Hapo hapana Myunani wala Myahudi, kutahiriwa wala kutokutahiriwa, mgeni wala mshenzi, mtumwa wala mwungwana, bali Kristo ni yote, na katika yote.” Unaona tunapaswa kuvaa utu mpya sawasawa na mfano wa yeye aliyetuumba, wakati wote ni lazima tulenge kuwa kama Yesu na kufanana naye.

7.       Tutatamani kumpendeza Yeye.

Ni muhimu kufahamu kuwa watu wanaopendana hutamani sana kufurahishana, sisi nasi ni muhimu kuhakikisha kuwa tunatamani kumpendeza Bwana wetu Yesu, yeye alitupenda upeo nasi hatuna budi kumpenda 2Wakoritho 5:14-15 “Maana, upendo wa Kristo watubidisha; maana tumehukumu hivi, ya kwamba mmoja alikufa kwa ajili ya wote, basi walikufa wote; tena alikufa kwa ajili ya wote, ili walio hai wasiwe hai tena kwa ajili ya nafsi zao wenyewe, bali kwa ajili yake yeye aliyekufa akafufuka kwa ajili yao.” Unaweza kuona haya ndio yalikuwa madai makubwa ya Bwana Yeye kuwa kila ambaye Mungu ni baba yake angampenda yeye maana yeye ametoka kwa Baba      Yohana 8: 42Yesu akawaambia, Kama Mungu angekuwa baba yenu, mngenipenda mimi; kwa maana nalitoka kwa Mungu, nami nimekuja; wala sikuja kwa nafsi yangu, bali yeye ndiye aliyenituma.”

Hitimisho:
Ukweli ulio wazi ni kuwa kama mtu hampenzi Yesu nasikitika kumjulisha mtu huyo kuwa maandiko yanasema amelaaniwa 1Wakoritho 16:22 “Mtu awaye yote asiyempenda Bwana, na awe amelaaniwa. Maran atha.” Na kwa sababu hiyo hii kama humpendi Yesu Mungu sio baba yako na kama Mungu sio baba yako wewe ni wa ibilisi na unawezaje kuwa mwana wa Mungu ni kwa imani kupitia Yesu Kristo, Wagalatia 3:26 “Kwa kuwa ninyi nyote mmekuwa wana wa Mungu kwa njia ya imani katika Kristo Yesu.” Ni kupitia yeye pekee tunaweza kumfikia Mungu na ndio maana Yesu aliwataka viongozi wa dini kuelewa wazi kuwa hawana budi kumkubali yeye endapo wanadai wanamjua Mungu lakini kama wanamkataa Yeye hawawezi kwa njia yoyote kuwa wana wa Mungu.

“Kama Mungu angekuwa baba yenu, mngenipenda mimi”

Rev. Innocent Kamote
Mkuu wa wajenzi mwenye Hekima.

Hakuna maoni: