Ijumaa, 16 Februari 2018

Je ! Mifupa hii yaweza kuishi?



Mstari wa Msingi: Ezekiel 37:1-3 “.Mkono wa Bwana ulikuwa juu yangu, naye akanichukua nje katika roho ya Bwana, akaniweka chini, katikati ya bonde; nalo limejaa mifupa; akanipitisha karibu nayo pande zote; na tazama, palikuwa na mifupa mingi katika ule uwanda! Nayo, tazama, ilikuwa mikavu sana.  Akaniambia, Mwanadamu, je! Mifupa hii yaweza kuishi? Nami nikajibu, Ee Bwana MUNGU, wajua wewe”.


Je! mifupa hii yaweza Kuishi?
Utangulizi:

Ni muhimu kufahamu kuwa Wana wa Israel walikuwa wameokolewa na Mungu kwa uweza mkubwa sana wote tunakumbuka jinsi Mungu alivyomuadhibu farao kwa mapigo mazito chini ya mkono wa Mtumishi wake Musa na Haruni, mpaka Mungu alivyojipatia taifa na kulistawisha katika nchi ya mkanaani na kuwa na ustawi mkubwa sana chini ya waamuzi na wafalme. Hata hivyo ni jambo la kusikitisha kuwa baada ya muda mfupi, walimuacha Mungu na kuabudu miungu na kumpuuzia Mungu aliyewaokoa, ukweli ni kuwa walisahau historia nzima na kugeukia njia zao, Hivyo Mungu aliruhusu waweze kwenda utumwani tena.

Mwaka kama wa 722BK na 586BK  Mungu aliruhusu Israel kuchukuliwa uhamishoni na Yuda kuchukuliwa uhamishoni Babeli chini ya utawala wa mfalme Nebuchadnezer, Jeshi la Nebuchadnezer liliizingira Yerusalem na kuharibu na kusambaratisha vibaya Hekalu lililokuwako Yerusalem na kulichoma moto kuwa majivu, na wayahudi walichukuliwa kwenda Utumwani Babeli, hiki ndio kilikuwa kifo cha Taifa hili na mwisho wa matumaini yao. Huu ulikuwa ni msiba mkubwa sana ambao haukuwa na matumaini ya kuupoza.

Daniel 1:1-4 “Katika mwaka wa tatu wa kumiliki kwake Yehoyakimu, mfalme wa Yuda, Nebukadreza mfalme wa Babeli,alikwenda Yerusalemu akauhusuru.Bwana akamtia Yehoyakimu, mfalme wa Yuda, katika mkono wake, pamoja na baadhi ya vyombo vya nyumba ya Mungu; naye akavichukua mpaka nchi ya Shinari, mpaka nyumba ya mungu wake; akaviingiza vile vyombo katika nyumba ya hazina ya mungu wake.  Mfalme akamwambia Ashpenazi, mkuu wa matowashi wake, awalete baadhi ya wana wa Israeli, wa uzao wa kifalme, na wa uzao wa kiungwana;  vijana wasio na mawaa, wazuri wa uso, wajuzi wa hekima, werevu kwa sababu ya maarifa yao, wenye kufahamu elimu, watakaoweza kusimama katika jumba la mfalme; tena alimwambia awafundishe elimu ya Wakaldayo, na lugha yao.    

Katika wakati huu watu wazuri na vijana wazuri na kila kitu kizuri kilichukuliwa utumwani Yerusalem ilibaki ukiwa huku kukiwa hakuna matumaini tena, Ezekiel nabii alikuwa ni miongozi mwa watu waliochukuliwa utumwani kwa mujibu wa historia.

Ni katika wakati huu sasa Ndipo Mungu alimwambia nabii Ezekiel katika maono aweze kuangalia bonde hili lisilo na matumaini, bonde lenye umauti usio na tumaini la kurejea tena na mifupa ilikuwa imetapakaa na ni mikavu hakukuwa na matumaini ya uhai na ndipo Mungu alipomuuliza Ezekiel swali hili Je mifupa hii mikavu yaweza kuishi?

Kwa ukweli maono haya yalikuwa yanalihusu Taifa la Israel kwa wakati huo kwa sababu walikuwa wamekata tamaa, walikuwa wamepoteza tumaini, waliona mauti na kujihisi kuwa ni kama wamekatiliwa mbali Ezekiel 37:11Kisha akaniambia, Mwanadamu, mifupa hii ni nyumba yote ya Israeli; tazama, wao husema, Mifupa yetu imekauka, matumaini yetu yametupotea; tumekatiliwa mbali kabisa.”ni kweli kuwa hakukuwa na namna na jinsi ya kujiokoa kutoka katika msiba huo, kwani watu wengi waliuawa na wengine walichukuliwa kwenda utumwani , Israel iilikuwa tayari limegeuka kuwa bonde lisilo na uhani, na ni lenye mauti sisyo na matumaini hii ilikuwa ni picha ya kukosekana kwa matumaini.

Tukio la jinsi hii lilijirudia tena Israel waliporudi tena kutoka utumwani, walipata Hekalu na Yesu alikuja lakinimnamo mwaka wa 70 hivi walitawanywa kotekote uhamishoni duniani na hakukuwa na matumaini tena na hekalu lilibomolewa lakini ilipofika 1948 Israel ilipata uhuru wake na kufanyika taifa tena Mungu ni mwaminifu kwa watu wake Historia inatushuhudia.

Hali hii sio tu kuwa ilikuwa inaihusu Israel wakati ule, lakini inawezekana ikawa inatuhusu sisi nasi katika siku hii ya leo, inawezekana uko mahali hapa unaisikia sauti hii, au unasoma makala hii, lakini ukiwa katika hali ya uzuni nzito inayokukabili, moyoni mwako ukiwa umepoteza matumaini, huoni nuru mbele matumaini yako yamepotea, una vyeti kadhaa vya madaktari, una shuhuda kadhaa za watu wenye tatizo kama lako na wote mmeambia kuwa tatizo lako haliwezekani, inawezekana ni wachawi wameharibu ukoo wenu, ni adui zako wamesema wale tumewaweza kwa hali hii hawachomoki tena, hawainuki tena uko katika giza nene, inawezekana watu wakakuona una-smile lakini Moyoni huna amani ya kweli, moyoni ni misiba, moyoni ni kukavu, hufurahii uwepo wa Bwana, unalia kilio cha ndani unajiuliza matumaini yatatokea wapi? Unajiuliza kehso itakuwaje? Unajiuliza nawezaje kukabiliana na aibu hii? Kila kitu kimesambaratika hakuna matumaini ya kusimama tena, ndoto zako zimeyeyuka? Mambo unayotaka ni kama hayaendi?

Namshukuru Mungu kwa Jibu alilolitoa Ezekiel 37:3bNami nikajibu Ee Bwana Mungu wajua wewe.” Ezekiel yuko katika Bonde lililojaa mifupa mikavu tena iliyotawanyika na kwaakili za kibinadamu hakuna uwezekano wa kuweko uzima wala ufufuo, ni vigumu kukubali hali halisi ya uzima hapa ni vigumu hata kufariji we ungejibuje swali kama hili, Lakini jibu la nabii Ezekiel linaonyesha kwa sehemu alijua kuwa Mungu anaweza kuwa anaelewa zaidi.

Ezekiel ni kama alikuwa anajua kuwa Mungu anaelewa zaidi, ni yeye pekee anayeweza kuingilia kati na kufanya kitu katika mazingira ambayo akili ya mwanadamu imefika mwisho, Ezekiel alikuwa anajua kuwa Mungu anaweza kufanya lolote analolitaka, kwa Mungu hakuna linaloshindikana, Mungu akitaka mifupa hii mikavu iiishi itaishi.

Mungu amenituma leo nikutangazie kuwa yasiyowezekana kwa wanadamu, Kwa Mungu yanawezekana kwake liko tumaini kubwa sana na hupaswi kukata tamaa, kila matumaini yanayofifia katika moyo wako na ndoto zako Bwana anaweza kukuinua tena Ee bwana Mungu wajua wewe ilikuwa ni sauti ya Ezekiel akimjibu Mungu ashukuriwe Mungu Ezekiel hakusema haiwezekani, lakini alisema Mungu anajua liko tumaini katika yeye, atakufufua tena atakupa uhai, kama alivyoipa Israel uhai, wa kisiasa na kiroho na kuliponya taifa lile na kulilinda hata liko tena leo.

Mungu atakuinua tena, Simama tena changamka usikae chini na kusikitika kuwa itakuwaje iko pumzi ya uhai leo, Bwana atakuganga kwa upya, kila kilicho na uhai na kisicho na uhai kinasikia neno la Mungu leo neno la Mungu linakuja kwako kama pumzi ya uhai nawe utajua ya kuwa Bwana ndiye Mungu Ezekiel 37:4-6Akaniambia tena, Toa unabii juu ya mifupa hii, uiambie, Enyi mifupa mikavu, lisikieni neno la Bwana. Bwana MUNGU aiambia mifupa hii maneno haya; Tazama, nitatia pumzi ndani yenu, nanyi mtaishi. Nami nitatia mishipa juu yenu, nami nitaleta nyama iwe juu yenu, na kuwafunika ngozi, na kutia pumzi ndani yenu, nanyi mtaishi; nanyi mtajua ya kuwa mimi ndimi Bwana.” 

Nakuomea ili kwamba Bwana afufue na kurejeza matumaini yako kila yanakoonekana kufifia aku kufa katika jina la Yesu Kristo wa Nazareth aliye hai.

Ni matumaini yangu kuwa umebarikiwa na ujumbe huu ningependa kupata maoni yako kama ujumbe huu umekubariki, na ni imani yangu utakubariki, au utabariki washirika wako usisite kumshukuru Mungu japo kwa ujumbe was sms

Rev. Innocent Kamote.

Mkuu wa Wajenzi mwenye Hekima.

0718990796        

Hakuna maoni: