Ijumaa, 3 Januari 2020

Yeye aliyetia Mkono wake Pamoja nani katika kombe ndiye atakaye nisaliti!


Mathayo 26:21-23. “Nao walipokuwa wakila, alisema, Amin, nawaambia, Mmoja wenu atanisaliti. Wakahuzunika sana, wakaanza kumwuliza mmoja mmoja, Ni mimi, Bwana? Akajibu akasema, Yeye aliyetia mkono wake pamoja nami katika kombe, ndiye atakayenisaliti.




Utangulizi:


Ndugu wapenzi leo kwa tuchukue muda kwa undani sana kuzungumzia kwa kina na mapana na marefu juu ya maneno haya ya msingi sana ya bwana wetu Yesu Kristo; Ufahamu kuhusu maneno haya ya hekima utamsaidia kila mmoja wetu katika kupunguza huzuni au kujiepusha na huzuni, zinazosababishwa na watu mbalimbali wanaotuzunguka hasa katika zamani hizi za uovu!

Aidha ufahamu wa kina na mapana kuhusu mstari huu au usemi huu wa muhimu sio tu utatusaidia kuweza kujilinda na watu wenye nia ovu wanaoweza kuyaathiri maisha yetu na tabia zetu na kutufanya kuwa na maisha mema au mabaya ya machungu au ya majuto lakini yatatusaidia kuwa na tahadhari dhidi ya watu wanaotusogelea kwa ukaribu kama ni wema au wabaya, Biblia inasema hivi kwa mfano katika 


Mithali 18:24 “Ajifanyiaye rafiki wengi ni kwa uangamivu wake mwenyewe; Lakini yuko rafiki aambatanaye na mtu kuliko ndugu.

 
Unaona maana yake nini kadiri tunavyokuwa na marafiki wengi zaidi, au kwa kadiri tunavyokuwa maarufu zaidi ndivyo tunavyojiweka katika hatari ya maangamizi zaidi, Maandiko yanatutaka tuwe macho na dunia na kuielewa vema usiishi duniani kana kwamba ni mahali salama sana, Dunia sio mahali salama hata kidogo, uwe umeoka uwe hujaokoka, uwe mtu mwema usiwe mtu mwema, dunia sio rafiki yako, ni lazima uishi kwa tahadhari!


Ni muhimu kufahamu na kuielewa vema dunia na kuijua ikoje ili uweze kuishi kwa amani, Kanisa au watu wa Mungu na pia watu wakarimu na wema, mara kadhaa wameshidhwa kuielewa dunia katika upana wake na matokeo yake wamejikuta wakilizwa, watu wengi sana wewe ni shahidi wamelizwa na watu waliokuwa karibu nao, wamelizwa na ndugu zao, wamelizwa na marafiki zao, wamelizwa na waume zao, wamelizwa na wake zao wamelizwa na watoto wao, wamelizwa na manabii, wamelizwa na maaskofu, wamelizwa na mashehe, wamelizwa na waganga wa kienyeji, wamelizwa na wapenzi wao, wamelizwa na wale waliowaamini na kuwaweka karibu na kuwapa siri zao kwa nini?  kwa sababu waliamini kila mtu na kufikiri kuwa dunia ni mahali salama ni  ndugu msomaji wangu ni makosa kufikiri hivyo !


Uishipo duniani ni lazima ukumbuke nasema tena ni lazima ukumbuke kuwa wewe ni kama kondoo katikati ya mbwa mwitu usisahau hilo 


Mathayo 10:16 “Angalieni, mimi nawatuma kama kondoo kati ya mbwa-mwitu; basi iweni na busara kama nyoka, na kuwa watu wapole kama hua

 
Haya ni maneno ya msingi sana ni ya muhimu mno kuyakumbuka, duniani kuna wanyama wa aina mbili, wako wanaokula majani na wako wanaokula nyama, wale wanaokula majani ni wapole sana na kazi yao kubwa ni kula majani, na wale wanaokula nyama ni wakali sana kazi yao ni kula wanyama wenzao, kama wewe ni mnayma unayekula majani unapokula majani ni lazima uinue kichwa chako na kujilinda ili wale wanaokula nyama wasikukule wewe, kwa sababu wakati wewe unakula nyasi kwa amani yuko mwindaji anaishi kwa kukukula wewe! Mwenye masikio ya kusikia na alisikie neno hili!


Yeye aliyetia mkono wake katika kombe ndiye atakayenisaliti!


Mathayo 26:23, “Nao walipokuwa wakila, alisema, Amin, nawaambia, Mmoja wenu atanisaliti. Wakahuzunika sana, wakaanza kumwuliza mmoja mmoja, Ni mimi, Bwana? Akajibu akasema, Yeye aliyetia mkono wake pamoja nami katika kombe, ndiye atakayenisaliti.


Turudi sasa katika mstari huuwa msingi ili kwamba tuweze kuuchambua sasa kwa kina na kujifunza kwanini Yesu alisema maneno haya! Na yana maana gani? Bila shaka utafahamu kusudi la Mungu kukufundisha jambo hili, Katika msatri huu kimsingi Yesu alikuwa akifundisha na kuweka wazi kuwa ataingizwa matatani na mtu aliye karubu sana atasalitiwa na mtu aliye rafiki, ataumizwa na mtu aliyemuamini sana ataumizwa na mtu aliyemjua vema sana rafiki aliye karibu, mtu aliyekula pamoja naye mezani pake!


Ni muhimu kufahamu kuwa nyakati za Biblia na katika tamaduni za kiyahudi hususani wakati walipokuwa wanakaribia sikukuu za Pasaka, walikuwa na desturi katika vyakula vyao kunakuwepo na chombo kidogo kilichoitwa “KOMBE” chombo hiki kilikuwa kinawekwa mboga chunguchungu zilizochanganywa na siki au vinegar  kwaajili ya kuongeza ugwaduugwadu katika chakula “appetizers” kule Tanga watu hutengeneza mbilimbi na kuzikatakata na kuweka pilipili na kuanika juani na inageuka kuwa siki na wakati wa kula siki huletwa karibu na kumiminwa katika kibakuli na kuchovya kwa kusudi la kula, kutokana na chombo hiki kuwa ni chombo muhimu sana kila mtu alikuwa na chombo chake na sio rahisi kushirikiana kuchovya katika chombo hicho, lakini kama mtu mmeshibana sana ni rafiki yako wa karibu na unamuamini kiasi cha kutokuogopa mate yake basi ungeweza kumruhusu achovyee kwenye chombo hicho unaweza kuona!


Kwa hiyo kimsingi, haikuwa lazima sana kuwa Yuda aliyemsaliti Yesu au watu fulani walichovya katika KOMBE lakini Yesu alikuwa anazungumzia ukaribu wa mtu atakaye msaliti kuwa ni yule ambaye alimuamini kwa kiwango cha kuruhusu atowelee tonge katika chombo chake unaweza kuona!


Yesu alikuwa anatutahadharisha kuwa shetani anaweza kumtumia mtu au watu waliokaribu kwa kiwango cha zaidi ya rafiki, na kuwa kama hatutachukua tahadhari tunaweza kujikutabtukiletewa au kufanyiwa madhara na watu waliokaribu au tuliowaamini kwa msingi huo ni vema ukawa makini sio tu na jamambazo na matapeli lakini vilevile wale wanaotuzunguka, watu wengi wana shuhuda za kuumizwa na wale walio karibu nao au wale waliowaamini, watu waliosomea maswala ya human intellectual na human intelligence wanasisitiza sana kuwa usimuamini mtu yeyote yule, wengi wamelizwa kwa kuwaamini na kujimwaga kichwakichwa kwa watu waliokuwa karibu nawe!  


Zaburi 41:9 “Msiri wangu tena niliyemtumaini, Aliyekula chakula changu, Ameniinulia kisigino chake.”


Lazima kila mwanadamu awe makini, ni lazima tujifunze na kuelewa kuwa wako watu watakaoonekana wanatupenda katika maisha yetu, wanaandamana nasi, wako nasi katika kila jambo jema na baya wanaokana kuwa rafiki, wanaonekana kutoa msaada ulio karibu lakini wanatusaliti wanatuuza kwa vipande thelathini vya fedha. Yuda alikuwa mwanafunzi muhimu katika wanafunzi wa Bwana Yesu alipatikana kwa maombi kama ilivyo kwa wengine Yesu alimuamini kwa kiwango cha kuwa mweka hazina wake 


Yohana 12:4-6 “Basi Yuda Iskariote, mmojawapo wa wanafunzi wake, ambaye ndiye atakaye kumsaliti, akasema, Mbona marhamu hii haikuuzwa kwa dinari mia tatu, wakapewa maskini? Naye aliyasema hayo, si kwa kuwahurumia maskini; bali kwa kuwa ni mwivi, naye ndiye aliyeshika mfuko, akavichukua vilivyotiwa humo.

 
Unaona Yesu alimuamini Yuda alimchagua awe miongoni mwa wasaidizi wake lakini huyu ndiye aliyemsaliti, huyu ndiye aliyemuingiza matatani na aliyemuingiza katika aibu kubwa sana na kubadilisha historia ya maisha ya Yesu, ilikuwa ni jambo la kusikitisha mno!


Kaka zangu dada zangu Neno la Mungu linatuonya kuwa tusimuamini mtu yeyote, sitaki unielewe vibaya kuhusu kuwa na marafiki, sitaki uninukuu vibaya kuhusu watu wanaokuzunguka lakini Neno la Mungu halidanganyi linasema ukweli na ukweli utabaki kuwa ukweli siku zote usimuamini mtu awaye yote adui wa mtu  ni watu wa nyumbani mwake mwenyewe angalia katika 


Mika 7:5-6 5. “Msimwamini rafiki, msimwekee kiongozi tumaini; ilinde milango ya midomo ya kinywa chako ili mkeo alalaye kifuani mwako asijue habari. Kwa maana mwana humwaibisha babaye, na binti huondoka ashindane na mamaye; na mwanamke aliyeolewa hushindana na mavyaaye; adui za mtu ni watu wa nyumbani mwake mwenyewe


Wako watu wamesalitiwa na rafiki zao, na wasiri wao, na wale waliokuwa karibu nao, wako watu wameibiwa na kutapeliwa kwa kuwaamini watu, wamejeruhiwa, na watu wa karibu zao, kwa kuwamini, watu wameozwa wanawake bomu kwa ushauri wa wachungaji wao,kwa ushauri wa wazazi wao, kwa ushauri wa shangazi zao, kwa ushauri wa rafiki zao, kwa ushauri wa watu wao wakaribu waliowaamini watu wameachwa na wachumba zao wakaolewa rafiki zao wa karibu waliowaamini, watu wamepinduliwa na mahause girl waliowatoa vijijini wakawathaminisha, watu wamesalitiwa na wachumba zao wake zao waliowasomesha,  watu wameharibiwa ndoa zao na wale waliokuwa karibu nao kama family friends, kuna vilio kila mahali kuna misiba kila mahali kuna kesi za wizi wa kuamini wa makahamani na polisi watu wakiwa wamedhulumiwa na watu waliowaamini, watu wameibiwa kwa njia ya simu na matapeli waliotumia namba za watu wanaowaamini, yeye aliyetia mkono wake katika kombe ndiye atakayenisaliti.


Wako watu wanaogopa leo kutoa hata lifti ya gari zao kwa watu wema kutokana na mambo yaliyowakuta, wako wachungaji walioumizwa na wale waliowaamini na kuwafanya kuwa wasaidizi wao, wako walioumizwa na rafiki zao, wako walicholonga misheni za kuibiwa kupitia rafiki zao, wako watu walikuja kugundua kuwa wake zao wamejenga mwakwao bila wao kujua, wako watu wamechomekewa na kulea watoto wasiokuwa wao, wako watu wamekodi teksi wakaibiwa, wako watu walomini nyumba za wageni wakaibiwa, 


Nataka kuchukua nafasi hii kukutia moyo wewe leo kuwa simama na Yesu, wanadamu waangalie mara mbilimbili, jihadhari nao, wanapokusifia angalia, wanaokuzunguka kuwa makini nao yeye aliyetia mkono wake katika kombe ndiye atakayenisaliti ni wale tuliowaamini kama afamily friends ndio baadaye walitembea na wake zetu, waume zetu, wale tuliowaamini kama ndugu wakalala katika vyumba na watoto wetu wa kiume ndio waliowalawiti, wale tuliowaonyesha tuliyo nayo ndio waliochonga mchongo tukaibiwa, wale waliotuoana tukitoa fedha bank ndio waliopigia simu majambazi. Watu wanaoweza kuharibu maisha yetu na kuyapa mwelekeo mwingine ni wale tuliowaamini, wako bodaboda wameuawa na hata kuporwa bodaboda zao wakifikiri wamepakiza watu wazuri, wako watu wametoa lifti kwa nia njema kwa watu wenye nia ovu na wakaingia matatani, wako watu wamepokea zawadi kwa watu waliowaamini wakajikuta wanatapeliwa, wako waliolizwa kwa majina ya viongozi wa kisiasa waliowaamini, Kanuni ya kibiblia inatutaka tusimuamini awaye yote kwa asilimia 100%.lakini tusiiishi kwa mashaka, Lakini tumuamini Mungu na kumuomba kila siku katika sehemu ile muhimu Yesu alitufundisha “USITUTIE MAJARIBUNI LAKINI UTUOKOE NA YULE MUOVU” Mungu atupe kuwa na macho ya rohoni na hekima na ujuzi kuhusu neno lake ili tusiwe miongoni mwa watu watakaoumizwa kwa wale tuliowaamini Yeye aliyetia mkono wake katika kombe ndiye atakayenisaliti.


Rev. Innocent Kamote
Mkuu wa wajenzi mwenye hekima!
0718990796

Hakuna maoni: