Jumamosi, 6 Novemba 2021

Kujengwa kwa Hekalu bila kelele!


1Wafalme 6:7. “Na nyumba ilipokuwa ikijengwa, ikajengwa kwa mawe yaliokwisha kuchongwa chimboni; wala nyundo, wala shoka, wala chombo cha chuma cho chote, sauti yake haikusikiwa ilipokuwa ikijengwa nyumba.”               

Utangulizi:

1Wafalme 6:7. “Na nyumba ilipokuwa ikijengwa, ikajengwa kwa mawe yaliokwisha kuchongwa chimboni; wala nyundo, wala shoka, wala chombo cha chuma cho chote, sauti yake haikusikiwa ilipokuwa ikijengwa nyumba”                

Moja ya mambo makubwa sana na ya kushangaza ya zamani ni pamoja na teknolojia waliyoitumia katika ujenzi. Uwezo wao na ustadi wao wa ujenzi ulikuwa ni wa hali ya juu sana, Hekalu la Suleimani limeingia katika orodha ya moja ya maajabu makubwa ya kale ya Dunia kutokana na ubora na uzuri wake, Ujenzi wake ulitawaliwa na utulivu mkubwa sana, tunasoma kwamba wakati Hekalu la ibada lililokuwa linajengwa na Sulemani, wajenzi walihakikisha kila pande la tofali linalohusika katika ujenzi, linachongwa mbali na eneo la ujenzi huko kware (Mgodini walikochonga mawe) walikuwa makini kuchonga kila jiwe kwa ufanisi mkubwa na jiwe lilipokuwa tayari, lilipelekwa eneo la ujenzi wa Hekalu na likajengwa bila kelele yoyote kusikika.

Mawe yaliyotumika hayakuwa madogo na wala hayakuwa na maruturutu yaani yalikuwa yamenyooka, waliyaleta mawe hayo yalikuwa makubwa, yalikuwa ya thamani sana ambayo yalikwishachongwa mgodini ona:-

1Wafalme 5:17-18 “Mfalme akaamuru, nao wakaleta mawe makubwa, mawe ya thamani, ili wauweke msingi wa nyumba kwa mawe yaliyochongwa. Na waashi wa Sulemani na waashi wa Hiramu na Wagebali wakayachonga, wakaweka tayari miti na mawe ya kuijenga nyumba.”

Mawe hayo ya thamani kubwa yalichongwa na kuandaliwa mgodini, mbali na eneo la ujenzi, kisha yakaletwa mjini wakayaweka tayari, Wajenzi wa Suleimani na Hiramu na Wagebali hawa walikuwa wataalamu maalumu wa shughuli ya ujenzi huo wa Hekalu.  

Katika namna zote mbili yaani kimwili na kiroho, uzuri na ufahari na taratibu za ujenzi wa Hekalu ulikuwa ni mradi unaosimamiwa na Roho Mtakatifu maandiko yako wazi kuwa sisi ni kazi ya Roho Mtakatifu.

Waefeso 2:19-22 “Basi tangu sasa ninyi si wageni wala wapitaji, bali ninyi ni wenyeji pamoja na watakatifu, watu wa nyumbani mwake Mungu.Mmejengwa juu ya msingi wa mitume na manabii, naye Kristo Yesu mwenyewe ni jiwe kuu la pembeni. Katika yeye jengo lote linaungamanishwa vema na kukua hata liwe hekalu takatifu katika Bwana. Katika yeye ninyi nanyi mnajengwa pamoja kuwa maskani ya Mungu katika Roho.”

Kila mtu aliyeokolewa ni hekalu la Roho Mtakatifu, kila mmoja ana thamani kubwa sana wote tumechongwa kwa jinsi ya kipekee mgodini na wote tumeletwa ili tuwe nyumba ya Mungu, na kuwa tumuabudu yeye na kuishi kwa amani bila malumbano wala mafarakano, kwa sababu kama mawe ya thamani kila mmoja lina thamani yake na linafaa kukaa pale lilipokusudiwa ona

1Petro 2:4-5“Mmwendee yeye, jiwe lililo hai, lililokataliwa na wanadamu, bali kwa Mungu ni teule, lenye heshima. Ninyi nanyi, kama mawe yaliyo hai, mmejengwa mwe nyumba ya Roho, ukuhani mtakatifu, mtoe dhabihu za roho, zinazokubaliwa na Mungu, kwa njia ya Yesu Kristo. Kwa kuwa imeandikwa katika maandiko Tazama, naweka katika Sayuni jiwe kuu la pembeni, teule, lenye heshima, Na kila amwaminiye hatatahayarika.       

1Wakorintho 3:16-17 “Hamjui ya kuwa ninyi mmekuwa hekalu la Mungu, na ya kuwa Roho wa Mungu anakaa ndani yenu? Kama mtu akiliharibu hekalu la Mungu, Mungu atamharibu mtu huyo. Kwa maana hekalu la Mungu ni takatifu, ambalo ndilo ninyi.”     

1Wakorintho 6: 19-20Au hamjui ya kuwa mwili wenu ni hekalu la Roho Mtakatifu aliye ndani yenu, mliyepewa na Mungu? Wala ninyi si mali yenu wenyewe; maana mlinunuliwa kwa thamani. Sasa basi, mtukuzeni Mungu katika miili yenu.”

Kwa hiyo tunakubaliana na maandiko kuwa kila aliyeokolewa ni Hekalu la Roho Mtakatifu na kwa umoja wetu ni jengo la Mungu na kila mmoja ni jiwe la thamani lililochongwa kwa ustadi, kutoka katika mgodi au kware ya giza iliyoko duniani na kuletwa na kuungamanishwa na Yesu Kristo ambaye ni jiwe kuu la pembeni, jiwe la msingi, hatujajichagua wenyewe bali ni Mungu ndiye aliyetuchagua  na kutuleta katika jengo lake, ili tumtukuze yeye na tena tumuabudu yeye na kumtumikia bila ya hofu yoyote.

Kwa nini hekalu halihitaji kelele?

Mungu amekusudia kutufanya sisi kuwa watu wake, na amekusudia kutupa utulivu, kelele asili yake ni huko mgodini, wakati wote unapotembelea mgodi au kware utasikia milipuko mikubwa ya kuvunjwa kwa mawe na mafundi wakitumia makrasha au mashine maalumu za kuvunja mawe, huko mafundi watayachonga mawe lakini yanapoletwa katika Hekalu yanakuwa tayari yanafaa kwa ujenzi, kelele zinawakilisha maisha ya duniani, kelele zinawakilisha taabu na uusumbufu wa kuwa nje ya uwepo wa Mungu, Kelele zinawakilisha hofu, kelele zinawakilisha kuwa uwepo wa Mungu umetoweka, kelele zinawakilisha hakuna ujenzi, bali kuna kuvunja vunja na kubomoa, na kuharibu.

Mahali kwenye hofu ya kifo, hofu ya utumwa hofu ya uvamizi, hofu ya uharibifu, hofu za maisha, hofu ya njaa, hofu ya kesho itakuwaje  ni mahali penye kelele  ni nje ya uwepo wa Mungu sio hekaluni, unapokuja kwenye uwepo wa Mungu Roho Mtakatifu tunapata utulivu wa ajabu na amani na tunatengwa mbali na kelele. Mungu amekusudia kumtenga kila mmoja wetu na kelele na kumpa kila mmoja wetu utulivu na amani.

Hutaogopa majeshi hodari yatatapopanga vita kwaajili yako Bwana anajua kuwa wewe ni hekalu lake kwa hiyo majeshi ya upinzani yatanyamazishwa, wakati wote Mungu Kama Mchungaji wetu hutuongoza katika maji ya utulivu

Zaburi 23:1-2, “Bwana ndiye Mchungaji wangu, Sitapungukiwa na kitu. Katika malisho ya majani mabishi hunilaza, kando ya maji ya utulivu huniongoza

Israel walipomlilia Musa kwa sababu ya Majeshi ya farao yaliyokuwa yakiwafuatia kwa nyuma ili kuwarejesha tena utumwani, Musa alitoa unabii ya kuwa Bwana atawapigania nao watanyamaza kimyaa! Mungu anafahamu ya kuwa wanadamu wanahitaji utuilivu wanahitaji ukimya! Wanahitaji amani, wanahitaji kuwa mbali na hofu, wanahitaji maisha ya ushindi, wanahitaji kuthibitishiwa kuwa watakuwa mbali na kelele za kila aina:-

Kutoka 14:13-14 “Musa akawaambia watu, Msiogope, simameni tu, mkauone wokovu wa BWANA atakaowafanyia leo; kwa maana hao Wamisri mliowaona leo hamtawaona tena milele. BWANA atawapigania ninyi, nanyi mtanyamaza kimya

Mungu atakustarehesha katika maskani yake utaburudishwa hata kutokee matetemeko, mafuriko sunami na mabadiliko yoyote yale sisi tunaokimbilia kwa Mungu kamwe hakuna atakayeogopa hakuna atakayetetemeshwa ukiwa katika uwepo wa Bwana ushindi unapatikana mapema asubuhi tu

Zaburi 46:1-5Mungu kwetu sisi ni kimbilio na nguvu, Msaada utakaoonekana tele wakati wa mateso. Kwa hiyo hatutaogopa ijapobadilika nchi, Ijapotetemeka milima moyoni mwa bahari. Maji yake yajapovuma na kuumuka, Ijapopepesuka milima kwa kiburi chake. Kuna mto, vijito vyake vyaufurahisha mji wa Mungu, Patakatifu pa maskani zake Aliye juu. Mungu yu katikati yake hautatetemeshwa; Mungu atausaidia asubuhi na mapema.”

Wewe unapokuwa Hekalu la Mungu huna sababu ya kupiga kelele, wala huna sababu ya kutikisika Mungu anafahamu wazi kuwa tunahitaji utulivu, tunahitaji kuwa kimya kisha yeye ataleta ukombozi, Daudi kila alipokuwa anakabiliwa na changamoto za aina mbalimbali alikumbuka anapaswa kutulia kimyaaaa na Mungu huyu yeye mwenyewe atazimaliza kelele

 Zaburi 62:1-2 “Nafsi yangu yamngoja Mungu peke yake kwa kimya, Wokovu wangu hutoka kwake. Yeye tu ndiye mwamba wangu na wokovu wangu, Ngome yangu, sitatikisika sana.”

Wanadamu hawapaswi kusumbuka, kama umechoshwa na kelele za dunia umechoshwa na wavunja mawe, kelele za kware, kelele za migodini wewe mfanye Bwana kuwa ndio mchungaji wako, utapata kila aina ya utulivu, utaandaliwa meza mbele za adui zako machoni pa watesi wako, hutakufa, hutaogopa mauti, utafarijiwa, utapata upako, nafsi yako itahuishwa, Baraka zitafurika nawe utakaa nyumbani mwa Bwana milele yaani kwenye utulivu!

Zaburi:23:1-6 “Bwana ndiye mchungaji wangu, Sitapungukiwa na kitu. Katika malisho ya majani mabichi hunilaza, Kando ya maji ya utulivu huniongoza. Hunihuisha nafsi yangu; na kuniongoza Katika njia za haki kwa ajili ya jina lake. Naam, nijapopita kati ya bonde la uvuli wa mauti, Sitaogopa mabaya; Kwa maana Wewe upo pamoja nami, Gongo lako na fimbo yako vyanifariji. Waandaa meza mbele yangu, Machoni pa watesi wangu. Umenipaka mafuta kichwani pangu, Na kikombe changu kinafurika. Hakika wema na fadhili zitanifuata Siku zote za maisha yangu; Nami nitakaa nyumbani mwa Bwana milele.”

Unapoona kelele maana yake nini?

Tunaweza kujibu kwa ufupi kuna uharibifu, mtu mmoja alisema kwa kiingereza hivi nanukuu “Destructive work is noisy, constructive work is silent” Kazi ya uharibufu ni ya kelele, na kazi ya ujenzi ni ya kimyakimya” Madhabahu ya Mungu ilikusudiwa pawe mahali pa ibada na hivyo katika torati Mungu aliagiza madhabahu isijengwe kwa kutumia chombo cha chuma yaani isichongwe! Kule kuchongwa kungeleata kelele ambazo Mungu hakutaka kuzisikia kupitia madhabahu yake au hekalu lake, kutumia chombo cha chuma kuichonga madhabahu au hekalu kungeweza kulitia unajisi hekalu!

Kumbukumbu 27:5-6“Na huko umjengee madhabahu Bwana, Mungu wako, madhabahu ya mawe, usitumie chombo cha chuma juu yake. Jenga hiyo madhabahu ya Bwana, Mungu wako, kwa mawe yasiyochongwa; ukamtolee Bwana, Mungu wako, sadaka za kuteketezwa juu yake;”

Kutoka 20:25 “Nawe ukinifanyia madhabahu ya mawe, hutaijenga ya mawe yaliyochongwa; kwa kuwa ukiwa wewe umetumia chombo chako katika kuichonga umeitia unajisi.”

Kwa hiyo unapoona kelele Katika ujenzi wa hekalu maana yake ni kuwa;-

# Watu wameacha kufanya kazi waliyoitiwa wanafanya biashara nyingine Marko 11:15-17 “Wakafika Yerusalemu, naye akaingia ndani ya hekalu, akaanza kuwafukuza wale waliokuwa wakiuza na kununua ndani ya hekalu, akazipindua meza za wabadili fedha, na viti vyao wauzao njiwa; wala hakuacha mtu achukue chombo kati ya hekalu. Akafundisha, akasema, Je! Haikuandikwa, Nyumba yangu itaitwa nyumba ya sala kwa mataifa yote? Bali ninyi mmeifanya kuwa pango la wanyang'anyi.”               

# Watu wakiwa mwilini, yaani udunia ukiingia, hekalu linakuwa na kelele 1Wakoritho 3:1-7  Lakini, ndugu zangu, mimi sikuweza kusema nanyi kama na watu wenye tabia ya rohoni, bali kama na watu wenye tabia ya mwilini, kama na watoto wachanga katika Kristo.Naliwanywesha maziwa sikuwalisha chakula; kwa kuwa mlikuwa hamjakiweza. Naam, hata sasa hamkiwezi, kwa maana hata sasa ninyi ni watu wa tabia ya mwilini. Maana, ikiwa kwenu kuna husuda na fitina, je! Si watu wa tabia ya mwilini ninyi; tena mnaenenda kwa jinsi ya kibinadamu? Maana hapo mtu mmoja asemapo, Mimi ni wa Paulo; na mwingine, Mimi ni wa Apolo, je! Ninyi si wanadamu? Basi Apolo ni nani? Na Paulo ni nani? Ni wahudumu ambao kwao mliamini; na kila mtu kama Bwana alivyompa. Mimi nilipanda, Apolo akatia maji; bali mwenye kukuza ni Mungu. Hivyo, apandaye si kitu, wala atiaye maji, bali Mungu akuzaye.”

#Watu wameingiwa na tamaa ona Yakobo 4:1-5 “Vita vyatoka wapi, na mapigano yaliyoko kati yenu yatoka wapi? Si humu, katika tamaa zenu zifanyazo vita katika viungo vyenu? Mwatamani, wala hamna kitu, mwaua na kuona wivu, wala hamwezi kupata. Mwafanya vita na kupigana, wala hamna kitu kwa kuwa hamwombi! Hata mwaomba, wala hampati kwa sababu mwaomba vibaya, ili mvitumie kwa tamaa zenu. Enyi wazinzi, hamjui ya kwamba kuwa rafiki wa dunia ni kuwa adui wa Mungu? Basi kila atakaye kuwa rafiki wa dunia hujifanya kuwa adui wa Mungu. Au mwadhani ya kwamba maandiko yasema bure? Huyo Roho akaaye ndani yetu hututamani kiasi cha kuona wivu?”

# Kila mtu anapokuwa na nia yake 1Petro 3:8-13 “Neno la mwisho ni hili; mwe na nia moja, wenye kuhurumiana, wenye kupendana kama ndugu, wasikitikivu, wanyenyekevu; watu wasiolipa baya kwa baya, au laumu kwa laumu; bali wenye kubariki; kwa sababu hayo ndiyo mliyoitiwa ili mrithi baraka. Kwa maana, Atakaye kupenda maisha, Na kuona siku njema, Auzuie ulimi wake usinene mabaya, Na midomo yake isiseme hila. Na aache mabaya, atende mema; Atafute amani, aifuate sana. Kwa kuwa macho ya Bwana huwaelekea wenye haki, Na masikio yake husikiliza maombi yao; Bali uso wa Bwana ni juu ya watenda mabaya. Naye ni nani atakayewadhuru, mkiwa wenye juhudi katika mema?”

# Watu wema wanaposhikamana na waovu 2Wakoritho 6:14-18 “Msifungiwe nira pamoja na wasioamini, kwa jinsi isivyo sawasawa; kwa maana pana urafiki gani kati ya haki na uasi? Tena pana shirika gani kati ya nuru na giza? Tena pana ulinganifu gani kati ya Kristo na Beliari? Au yeye aaminiye ana sehemu gani pamoja na yeye asiyeamini? Tena pana mapatano gani kati ya hekalu la Mungu na sanamu? Kwa maana sisi tu hekalu la Mungu aliye hai; kama Mungu alivyosema, ya kwamba, Nitakaa ndani yao, na kati yao nitatembea, nami nitakuwa Mungu wao, nao watakuwa watu wangu. Kwa hiyo, Tokeni kati yao, Mkatengwe nao, asema Bwana, Msiguse kitu kilicho kichafu, Nami nitawakaribisha. Nitakuwa Baba kwenu, Nanyi mtakuwa kwangu wanangu wa kiume na wa kike,”

# Mbinguni hakutaingia chochote kilicho kinyonge

Ujenzi huu wa ajabu ambapo mawe yalikuwa yakichongwa mbali, huko kware au mgodini, yaliletwa katika kiwanja cha hekalu yakiwa yamekamilika unatukumbusha wazi kuwa shemu ya kuchongwa watu ni hapa duniani, Roho Mtakatifu hufanya maandalizi ya kutuandaa na kutuchonga tukiwa hapa Duniani, anatukarabati ndani na nje ili tufae kuwa chombo cha sifa na ibada lakini zaidi  kwamba baadaye tuweze kufika Mbinguni ambako huko ni eneo la utulivu na hakuna kuchongwa tena tutaingia tukiwa tumekamilishwa baada ya kupitia mchakato wa utakatifu duniani kule mbinguni hakuna chochote kilicho kinyonge kitakachoingia,

Wafilipi 1:6 “Nami niliaminilo ndilo hili, ya kwamba yeye aliyeanza kazi njema mioyoni mwenu ataimaliza hata siku ya Kristo Yesu;”

kila mmoja anapaswa kujiweka wakfu kwa maneno kama yale ambayo Suleimani aliyasema siku alipokuwa akiliweka wakfu Hekalu, alisema

1Wafalme 8:13 Hakika nimekujengea nyumba ya kukaa, iwe mahali pa makao yako milele. Meno ya kiingereza ya mstari huu ni matamu zaidi kwani yanasema hivi “I have indeed built you exalted house, a place for you to dwell in forever” Mungu anataka tuwe makazi yake milele.

Rev. Innocent Samuel Kamote

Mkuu wa wajenzi mwenye Hekima!

Hakuna maoni: