Jumanne, 29 Machi 2022

Na sisi je tufanye nini?


Luka 3:2-14wakati wa ukuhani mkuu wa Anasi na Kayafa, neno la Mungu lilimfikia Yohana, mwana wa Zakaria, jangwani. Akafika nchi yote iliyo karibu na Yordani, akihubiri ubatizo wa toba liletalo ondoleo la dhambi, kama ilivyoandikwa katika chuo cha maneno ya nabii Isaya; Sauti ya mtu aliaye nyikani, Itengenezeni njia ya Bwana, Yanyosheni mapito yake. Kila bonde litajazwa, Na kila mlima na kilima kitashushwa; Palipopotoka patakuwa pamenyoka, Na palipoparuza patalainishwa; Na wote wenye mwili watauona wokovu wa Mungu. Basi, aliwaambia makutano ya wale waliomwendea ili awabatize, Enyi wazao wa nyoka, ni nani aliyewaonya ninyi kuikimbia hasira itakayokuja? Basi, toeni matunda yapatanayo na toba; wala msianze kusema mioyoni mwenu, Tunaye baba, ndiye Ibrahimu; kwa maana nawaambia ya kwamba katika mawe haya Mungu aweza kumwinulia Ibrahimu watoto. Na sasa hivi shoka limekwisha kuwekwa penye mashina ya miti; basi kila mti usiozaa matunda mazuri hukatwa na kutupwa motoni. Makutano wakamwuliza, Tufanye nini basi?  Akawajibu akiwaambia, Mwenye kanzu mbili na ampe asiye na kanzu; na mwenye vyakula na afanye vivyo hivyo. Watoza ushuru nao wakaja kubatizwa, wakamwuliza, Mwalimu, tufanye nini sisi?  Akawaambia, Msitoze kitu zaidi kuliko mlivyoamriwa. Askari nao wakamwuliza, wakisema, Sisi nasi tufanye nini? Akawaambia, Msidhulumu mtu, wala msishitaki kwa uongo; tena mtoshewe na mshahara wenu.”

Utangulizi:

Moja ya manabii wa ajabu sana ambao unaweza kujifunza habari zao na ukashangaa ni pamoja na na Nabii Yohana mbatizaji, Huduma yake ya kinabii ilikuwa imejawa na kuwaandaa watu watubu, kwaajili ya kumpokea Masihi, Ni wazi kuwa Masihi kwa namna anavyoelezewa na maandiko ni kiongozi wa ngazi ya juu mno na ambaye sio wa kawaida na hivyo Mungu aliona kuwa hawezi kupokelewa kienyeji bila mioyo ya watu kuandaliwa ili iweze kustahimili ujio wa Masihi, kwa hiyo Mungu katika mpango wake alikusudia kumtuma Yohana Mbatizaji nabii, Hili linadhihirishwa wazi na nabii Isaya miaka 700 kabla ya ujio wa Yesu, alitabiri juu ya ujio wa Yohana mbatizaji na huduma yake ambayo ilikuwa na umuhimu mkubwa sana katika kuandaa mazingira ya kumpokea Yesu Duniani ona:-  

Isaya 40:3-5 “Sikiliza, ni sauti ya mtu aliaye, Itengenezeni nyikani njia ya Bwana; Nyosheni jangwani njia kuu kwa Mungu wetu. Kila bonde litainuliwa, Na kila mlima na kilima kitashushwa; Palipopotoka patakuwa pamenyoka, Na palipoparuza patasawazishwa; Na utukufu wa Bwana utafunuliwa, Na wote wenye mwili watauona pamoja; Kwa kuwa kinywa cha Bwana kimenena haya.”

Unaweza kuona umuhimu wa nabii huyu ulikuwa mkubwa mno, kwani alitumwa kuwaandaa watu watubu kabla ya huduma ya masihi kwa kuwa masihi mwenyewe ndio wokovu wa Bwana utakaofunuliwa kwa watu kwa jinsi ya Mwili, Masihi mwenyewe ni utukufu wa Mungu, na kwa sababu watu wangemuona kwa macho yao ya mwili ilikuwa ni muhimu kuandaa mioyo yao ili macho yao yauone wokovu wa Bwana na utukufu utakaofunuliwa kwa watu wote ona:-

Luka 2:25-32 “Na tazama, pale Yerusalemu palikuwa na mtu, jina lake Simeoni, naye ni mtu mwenye haki, mcha Mungu, akiitarajia faraja ya Israeli; na Roho Mtakatifu alikuwa juu yake. Naye alikuwa ameonywa na Roho Mtakatifu ya kwamba hataona mauti kabla ya kumwona Kristo wa Bwana. Basi akaja hekaluni ameongozwa na Roho; na wale wazazi walipomleta mtoto Yesu ndani, ili wamfanyie kama ilivyokuwa desturi ya sheria,yeye mwenyewe alimpokea mikononi mwake, akamshukuru Mungu, akisema, Sasa, Bwana, wamruhusu mtumishi wako, Kwa amani, kama ulivyosema; Kwa kuwa macho yangu yameuona wokovu wako, Uliouweka tayari machoni pa watu wote;Nuru ya kuwa mwangaza wa Mataifa, Na kuwa utukufu wa watu wako Israeli.”

Kuja kwa Masihi kuliambatana na mahubiri mazito yaliyokuwa yakiwataka watu wawe na toba ya kweli iliyoambatana na kuzaa matunda na kubatizwa ili kudhihirisha kuwa kweli watu wamebadilika na wako tayari kumpokea Masihi, ilikuwa ni lazima jamii iwe na usafi wa moyo na kuwa mioyo yao ilikuwa lazima iwe tayari kwaajili ya Mungu na kwaajili ya wanadamu, Ili Yesu akute na atembelee jamii ilikuwa ni lazima njia isafishwe, palipo na kilima pasawazishwe na kila mahali ambako hakuko sawa sawa ilikuwa ni lazima pawe sawa, kila kikwazo ilikuwa ni lazima kiondolewe ili watu waweze kuishuhudia neema ya Mungu maishani mwao, ilikuwa ni lazima watu wawe mbali na uchungu, waondoe chuki dhidi ya Mungu, na maudhi na kero zote walizokuwa wakiwafanyia wanadamu wenzao, Yohana aliwaonya juu ya hukumu ya Mungu itakayokuja endapo kizazi kile hakitatubu, Hata hivyo ujumbe wa Yohana mbatizaji ulikuwa na mtindo wenye kufurahisha sana kwa sababu watu walimwendea wakitubu kwa kupitia kazi zao (professional), Mtindo wake wa kimaonyo na kimahubiri unaonyesha wazi kuwa ni watu ndio walimuendea wenyewe wakitubu, na kuuliza maswali, lakini sio hivyo watu walienda kimakundi kutokana na uhalisia wa kazi zao na kila mmoja akitaka kujua kuwa afanyaje ili asimkwaze Mungu na jamii na ndio maana swali kubwa la ujumbe huu ni *Na sisi je tufanye nini?*

1.       Kwa Jamii (Makutano) – Yohana mbatizaji alishangaaa kuona jamii kubwa ya watu wakikimbia kwenda kutubu na hivyo aliiambia jamii waziwazi, Kwamba waondoe uchungu mioyoni mwao Luka 3:7 “Basi, aliwaambia makutano ya wale waliomwendea ili awabatize, Enyi wazao wa nyoka, ni nani aliyewaonya ninyi kuikimbia hasira itakayokuja?Kitendo cha kuwaita makutano kizazi cha nyoka kilimaanisha kuwa watu wengi walikuwa upande wa shetani ambaye ndiye nyoka, lakini sio hivyo tu jamii ilikuwa na uchungu na malalamiko ya kila aina, na sio hivyo tu ilikuwa ni jamii iliyojaa hila na dhuluma na vilio vya kila aina, manung’uniko na hali ya kujiona kuwa hawakufanyiwa sawa, watu ambao wakati wote hawana jema Yohana aliwaonya watu wa namna hii Kuwa kamwe hawatafurahia uwepo wa Masihi, Na ujio wa Masihi hautakuwa na maslahi wa jamii yenye uchungu, jamii yoyote yenye uchungu hata uwafanyie nini hawatakuja kuridhika hata siku moja, hawatakuja kutoa shukurani, wakati wote watalalamika, uwepo wa Mungu na Baraka za Mungu na Hazifanyi kazi kwa jamii ambayo imejaa uchungu, Na ndio maana Yoaha nanakiita kizazi cha nyoka!Uchungu wakati wote katika maisha unapunguza sana neema ya Mungu, Maandiko yanatuonya kutokuwa na uchungu!

 

Waebrania 12:15 “mkiangalia sana mtu asiipungukie neema ya Mungu; shina la uchungu lisije likachipuka na kuwasumbua, na watu wengi wakatiwa unajisi kwa hilo.”

 

Yohana alikuwa anaiona hukumu ya Mungu na kuwa mafanikio hayawezi kuja kwa jamii ambayo wakati wote inalalamika tu au kwa jamii ambayo haitendeani mema au kwa jamii iliyojaa dhuluma, wizi, ubabaishaji, na hila za kila aina au jamii ambayo hairushusu hofu ya Mungu kutawala! Kama jamii ina uchungu wa aina yoyote hicho ni kizazi cha nyoka!

 

Waefeso 4:31-32 “Uchungu wote na ghadhabu na hasira na kelele na matukano yaondoke kwenu, pamoja na kila namna ya ubaya; tena iweni wafadhili ninyi kwa ninyi, wenye huruma, mkasameheane kama na Mungu katika Kristo alivyowasamehe ninyi.”

 

Kizazi cha nyoka ni jamii iliyojawa na uchungu na uchungu ni sumu, ghadabu, hasira ni lazima iondoke katika jamii, uovu na ubaya wa kila namna ni lazima uondoke katika jamii ambayo inamtaka Masihi awe kiongozi wao, apite katikati yao aweze kuwa Baraka na kuleta uponyaji, ni lazima iwe jamii inayojaliana na kufadhiliana jamii ambayo imeacha umimi ubinafsi na uchoyo, Maandiko yanaitaka jamii kuondoa uchungu kwa kujilinda na choyo na kufadhiliana ona

 

Luka 12:15 “Akawaambia, Angalieni, jilindeni na choyo, maana uzima wa mtu haumo katika wingi wa vitu vyake alivyo navyo.”

 

Si vema Yesu akaja katika jamii na kuikuta ina sumu, ina uchungu, na hasira, ina ubaya ina uovu, ina hali ya kutokusameheana au  isiyosamehe, jamii inayosingiziana, Yesu anaitaka jamii iwe na fadhili na ndio maana Yohana mbatizaji aliiiambia jamii kama una cha ziada gawia wasio nacho !

 

Luka 3:10-11 “Makutano wakamwuliza, Tufanye nini basi? Akawajibu akiwaambia, Mwenye kanzu mbili na ampe asiye na kanzu; na mwenye vyakula na afanye vivyo hivyo

 

Jamii isiyo na umimi itajifunza kutoa na kufadhiliana na itaachana na ubinafsi na kuangaliana wao kwa wao, leo hii jamii haiko hivyo kila mtu ana uchungu na kila mtu yuko kwenye kujikusanyia, kila mtu anangalia mambo yake na tumekuwa na jamii isiyo na shukurani na bingwa wa kulalamika na kujenga hoja za malalamishi ndio anaonekana shujaa katika jamii! Kama jamii ikiwa katika hali hiyo kweli hicho ni kizazi cha nyoka na hakina budi kubadilika na kutoka katika hali ya kuwa wana wa ibilisi na kuwa wana wa Mungu!

 

2.       Mafarisayo na Masadukayo (Madhehebu mbalimbali) – Wakati wa Yohana mbatizaji na Yesu pia kulikuwa na watu wa Madhehebu ya aina mbalimbali, madhehebu makubwa ya watu waliokuwepo nyakati hizo walikuwa ni pamoja na Mafarisayo na masadukayo, hawa walikuwa madhehbu maarufu sana nao waliposikia huduma ya Yohana mbatizaji walimwendea na wakatubu kwa wingi lakini Yohana hakuwaacha bila maonyo watu wa Madhehebu aliwaonya kuwa ni lazima waache kiburi cha kidini na kidhehebu, lakini lazima waache kujihesabia haki, Mafarisayo na Masadukayo walijifikiri kuwa wao ni madhehebu bora kwa sababu Ibrahimu ni baba yao Mbatizaji aliwaonya kwa manenio haya ona:-

 

Mathayo 3:7-10 “Hata alipoona wengi miongoni mwa Mafarisayo na Masadukayo wakiujia ubatizo wake, aliwaambia, Enyi wazao wa nyoka, ni nani aliyewaonya ninyi kuikimbia hasira itakayokuja? Basi zaeni matunda yapasayo toba; wala msiwaze mioyoni mwenu kwamba, Tunaye baba, ndiye Ibrahimu; kwa maana nawaambia ya kwamba Mungu aweza katika mawe haya kumwinulia Ibrahimu watoto. Na shoka limekwisha kuwekwa penye mashina ya miti; basi kila mti usiozaa matunda mazuri hukatwa na kutupwa motoni.”

 

Mafarisayo na masadukayo yalikuwa ni madhehebu makubwa nyakati za Yohana na Masihi, Mafarisayo katika theolojia yao walikuwa wakiamini katika ufufuo wa wafu, waliamini katika malaika na maono na walikubaliana na vitabu vya Musa na manabii, lakini Masadukayo wao hawakuamini katika ufufuo, wala hawakuamini katika malaika na maono na waliamini vitabu vitano vya Musa tu na hawakujali vitabu vya manabii, kila mmoja alikuwa akijiona bora kutokana na madhehebu yake aliyokuwa nayo,Lakini zaidi sana walidhani ya kuwa Mungu anawahesabia haki kwa vile wao ni wana wa Ibrahimu, hata leo katika jamii zetu watu wanadhani kuwa kuwa na madhehebu ndio kuuchinja, wananadi sana madhehebu yao kuliko kumnadi Yesu, Yohana Mbatizaji aliwakazia akawaambia sikiliza Mungu anataka matunda yatokanayo na toba, Mungu anataka watu waliotubu na kugeuka na kuacha dhambi, ishu sio kuwa mtoto wa Ibrahimu kwa sababu Mungu anaweza kumuinulia Ibrahimu watoto hata kutoka katika mawe, Hivyo Dhehebu lako sio ishu wala sio dili, dili ni Yesu, Dili ni Masihi, dili ni toba ya kweli na mabadiliko, Mungu anataka matunda mazuri, hakuna matunda mazuri mti huo utakatwa na kutupwa motoni:-

 

Wagalatia 5:19-24 “Basi matendo ya mwili ni dhahiri, ndiyo haya, uasherati, uchafu, ufisadi, ibada ya sanamu, uchawi, uadui, ugomvi, wivu, hasira, fitina, faraka, uzushi, husuda, ulevi, ulafi, na mambo yanayofanana na hayo, katika hayo nawaambia mapema, kama nilivyokwisha kuwaambia, ya kwamba watu watendao mambo ya jinsi hiyo hawataurithi ufalme wa Mungu. Lakini tunda la Roho ni upendo, furaha, amani, uvumilivu, utu wema, fadhili, uaminifu, upole, kiasi; juu ya mambo kama hayo hakuna sheria. Na hao walio wa Kristo Yesu wameusulibisha mwili pamoja na mawazo yake mabaya na tamaa zake.”

 

Wakati Yohana akikazia kuwa shoka limekwisha kuwekwa tayari na ni moto tu unahusu watu wasio na toba Paulo anaongezea kuwa watu wenye matunda yasiyofaa hawatauona ufalme wa Mungu, Kama una dini nzuri watu wanataka kuona matendo yako na sio vinginevyo, kama una dhehebu zuri watu wanataka kuona mabadiliko dini au dhehebu lako halitusaidiii katika jamii Mungu anataka matunda kinyume cha hapo ni hukumu tu. Wayahudi na waislamu na wakristo wanatokana na Imani ya Ibrahimu na wote wanakiri kuwa Ibrahimu nabii ni baba yao wa imani, Ni muhimu kufahamu kuwa dini na madhehebu hayatatusaidia kama hakuna matunda ya kweli na toba ya kweli

 

Yakobo 1:26-27 “Mtu akidhani ya kuwa anayo dini, wala hauzuii ulimi wake kwa hatamu, hali akijidanganya moyo wake, dini yake mtu huyo haifai. Dini iliyo safi, isiyo na taka mbele za Mungu Baba ni hii, Kwenda kuwatazama yatima na wajane katika dhiki yao, na kujilinda na dunia pasipo mawaa.”

 

Kwa msingi huo Yohana aliionya jamii kuacha kujivunia dini zao na Madhehbu yao, wako watu ambao wako tayari kufa kwaajili ya dini zao wanazing’ang’ania kama chapati na hawana mpango na Yesu, na sio hivyo tu wanakiri ya kuwa wana dini lakini matunda hayaonekani, kama watu wana dini ya kweli chuki inatoka wapi, majungu yanatoka wapi, kiburi na dharau kinatoka wapi, fitina na majungu na kujipendekeza kunatokea wapi?  Mbona watu hawajilindi na mawaa, mbona hawajilindi na dunia, mtu anakiri kuwa na dhehebu safi lakini amejaaa viwango vya kidunia. Ni lazima watu watubu na kuzaa matunda.Vinginevyo hukumu itamhusu kila mmoja bila kujali ana dhehebu au dini nzuri kiasi gani!

 

3.       Watoza ushuru - Luka 3:12-13 “Watoza ushuru nao wakaja kubatizwa, wakamwuliza, Mwalimu, tufanye nini sisi? Akawaambia, Msitoze kitu zaidi kuliko mlivyoamriwa.”

 

Kundi hili nalo wakati wa Yohana mbatizaji lilijitokeza kutubu, hawa walikuwa ni watoza ushuru, kundi hili liliagizwa kuacha dhuluma na kutoza zaidi ya kiwango kilichowekwa, kundi hili lilikuwa ni kundi la watu wenye tamaa ya fedha na waliojilimbikizia mali ka njia ya dhuluma, Dhambi yao kubwa ilikuwa ni kuzidisha na kutoza zaidi ya jinsi ilivyoamuriwa  ni watu waliokuwa wamejaa dhuluma sana, waliwadhulumu wananchi lakini pia hawakufikisha mapato serikalini, jamii ya watoza ushuru walihesabika kuwa hawana uzalendo na wala wakati mwingine sio waaminifu na hawafikishi kile kiwango cha fedha wanachokusanya au wakati mwingine walitoza juu ya kiwango kwa faida zao wenyewe! Hwa pia waliongezea manung’uniko katika jamii na kwa wayahudi watu hawa waliwekwa katika kundi la watu wenye dhambi sana, Kundi hili pia lilitakiwa kuacha uovu wake na kujiandaa kumpokea Yesu

 

 Luka 19:2-10 “Na tazama, palikuwa na mtu, jina lake Zakayo, mkubwa mmoja katika watoza ushuru, naye ni tajiri. Huyu alikuwa akitafuta kumwona Yesu ni mtu wa namna gani, asiweze kwa sababu ya umati wa watu, maana ni mfupi wa kimo. Akatangulia mbio, akapanda juu ya mkuyu apate kumwona, kwa kuwa atakuja kuipitia njia ile. Na Yesu, alipofika mahali pale, alitazama juu, akamwambia, Zakayo, shuka upesi, kwa kuwa leo imenipasa kushinda nyumbani mwako. Akafanya haraka, akashuka, akamkaribisha kwa furaha. Hata watu walipoona, walinung'unika wote, wakisema, Ameingia kukaa kwa mtu mwenye dhambi. Zakayo akasimama, akamwambia Bwana, Tazama, Bwana, nusu ya mali yangu nawapa maskini, na ikiwa nimenyang'anya mtu kitu kwa hila namrudishia mara nne.Yesu akamwambia, Leo wokovu umefika nyumbani humu, kwa sababu huyu naye ni mwana wa Ibrahimu. Kwa kuwa Mwana wa Adamu alikuja kutafuta na kuokoa kile kilichopotea.”

 

Watoza ushuru walikuwa wamejitajirisha kupitia mali za dhuluma, na kuzidisha kiwango cha fedha kilichowekwa, hawa Yohana mbatizaji aliwajibu walipo uliza na sisi je tufanye nini aliwaambia wasitoze zaidi ya kiwango kilichowekwa, sehemu nyingi sana leo hii kumekuweko na watu ambao wanatoza zaidi ya kiwango kilichowekwa, unadhani kwanini serikali inapiga marufuku swala la twisheni kwa walimu? Kwa sababu tayari ada zipo zimewekwa, lakini kwanini walimu wanafanya twisheni, kwa nini wanachukua fedha ili wakufundishe pembeni pembeni, ada unayolipa haiwatoshi? Kuna namna nyingi sana watu wanatoza zaidi ya kiwango kilichowekwa,  wako pia wafanya biashara ambao wanatoza zaidi ya kiwango kinachokusudiwa na ukitaka kuwaweza we sema tu unadai risiti, watakuambia kuna bei ya kuandika kwenye risiti na bei ya bila risiti, Kristo hawezi kukubaliana na jamii ya watu yenye dhuluma ili aweze kuweka makazi anahitaji watu watubu kama alivyofanya Zakayo, aliamua kutubu na kurudhisha kwa jamii kile alichokusanya, wako watu wanakusanya na hawarudishi kwa jamii, lakini vilevile hawafikishi serikalini kama kila aina ya ushuru ungekuwa unafika inakotakiwa serikali ingekuwa imepiga hatua kubwa sana ya maendeleo, watu wangeweza kunufaika na mataifa yao na nchi zao na huduma za kijamii bila kuhitaji kukopa katika mataifa au mabenki, hakungekuwa na sababu ya kuinamia mataifa mengine, kuhitaji msaada, watoza ushuru hali kadhalika walifanya kazi za kubambikizia watu kodi nzito, kutishia kufunga biashara ugomvi na wafanya biashara dhuluma na mambo mengine ya kusikitisha lakini hata hivyo wakitubu Yesu atawapokea.

 

4.       Askari – Luka 3:14 “Askari nao wakamwuliza, wakisema, Sisi nasi tufanye nini? Akawaambia, Msidhulumu mtu, wala msishitaki kwa uongo; tena mtoshewe na mshahara wenu

 

Maandiko hayaonyeshi kuwa kazi ya uaskari kuwa ni kazi mbaya au isiyofaa kwani ni wazi Askari waliomjia Yohana mbatizaji hapa ilikuwa ndio mahali pa kuwaambia waache kabisa kazi hiyo kama ingekuwa haifai, katika ulimwengu huu ulioharibika askari ni wa Muhimu na wanahitajika kwa sababu kuna watu ni waizi, na bila kuweko askari wakati mwingine ni ngumu kuitunza amani inayokusudiwa, Lazima askari wawepo ili kukomesha umwagikaji mkubwa wa damu na kuzuia uhalifu, kulinda taifa raia na mali zao na kuhakikisha usalama unakuwepo kila eneo, hivyo nabii hakusema waache kazi hii lakini aliwaonya wasidhulumu mtu na wala wasishitaki mtu kwa uongo kubambikizia watu kesi na kuwa watosheke na mishahara yao,Jaribu hili ndilo lililokuwa likiwakabili askari na hasa jeshi la polisi ambao walikuwa wakilinda usalama wa raia na mali zao katika mswala haya matatu kuna mambo ya ksingi ya kujifunza kwetu kwa kila kitu walichojibiwa askari kupitia Yohana mbatizaji.Sisi ni aksari tufanye nini:-

 

1.       Msimdhulumu mtu.

 

Dhuluma kwa kiingereza maana yake ni “unrighteousness” au KAKIA kwa kiyunani yaani ni hali ya kutokutenda haki, kutenda kwa ubaya, kutenda kwa kuumiza, kutenda bila kujali, watu wengi sana hawatendi haki hususani askari na hata watu wasio askari, lakini hata hivyo neno la Mungu linamtaka kila mtu atende haki kutokutenda haki kunaondoa neema ya Mungu

 

Tito 2:11-12 “Maana neema ya Mungu iwaokoayo wanadamu wote imefunuliwa; nayo yatufundisha kukataa ubaya na tamaa za kidunia; tupate kuishi kwa kiasi, na haki, na utauwa, katika ulimwengu huu wa sasa;”

 

Kutokutenda haki sio mpango wa Mungu, Mungu alimwita Abrahamu ili awafundishe watu wake kutenda haki, na hii ndio sababu kubwa kwa nini Mungu alimchagua Ibrahimu, Mungu mwenyewe anaeleza:-

 

Mwanzo 18:17-19 “BWANA akanena, Je! Nimfiche Ibrahimu jambo nilifanyalo, akiwa Ibrahimu atakuwa taifa kuu, hodari, na katika yeye mataifa yote ya dunia watabarikiwa? Kwa maana nimemjua ya kwamba atawaamuru wanawe, na nyumba yake baada yake waishike njia ya BWANA, wafanye haki na hukumu, ili kwamba BWANA naye akamtimizie Ibrahimu ahadi zake.”

 

Mungu hukasirishwa sana wanadamu wanapoacha kutenda haki na kufadha udhalimu

 

Warumi 2:18 “Bali kwa kadiri ya ugumu wako, na kwa moyo wako usio na toba, wajiwekea akiba ya hasira kwa siku ile ya hasira na ufunuo wa hukumu ya haki ya Mungu, atakayemlipa kila mtu kwa kadiri ya matendo yake; wale ambao kwa saburi katika kutenda mema wanatafuta utukufu na heshima na kutokuharibika, watapewa uzima wa milele;     na wale wenye fitina, wasioitii kweli, bali wakubalio dhuluma, watapata hasira na ghadhabu;”

 

Na ndio maana sasa katika mahubiri ya Yohana Mbatizaji aliwataka askari kuhakikisha kuwa hawadhulumu mtu na hii ilikuwa ni agizo la kwanza kwao haki huinua taifa bali dhambi ni aibu ya taifa zima !

 

2.       Wala msimshitaki mtu kwa uongo:

 

Kushitaki watu kwa uongo ni moja ya dhambi kubwa sana zinazofanywa na askari Katika Biblia mara kadhaa tumewahi kushuhudia watu wakiuawa na kuhukumiwa kwa kusingiziwa makosa yasiyokuwa yao, siku hizi unaweza kupewa kesi nzito kama Uhaini, unaweza kubambikiziwa ugaidi, au utakatishaji wa fedha au uhujumu uchumi na kadhalika kesi ambazo zinaweza kukunyima dhamana na ukajikuta unasota rumande Moja ya amri katika amri za Mungu ni pamoja na kutokushuhudia uongo

 

Kutoka 20:16 “Usimshuhudie jirani yako uongo”. Ni wazi kuwa kwa mujibu wa sheria za Musa kushuhudia uongo lilikuwa ni moja ya makosa mazito na kama mtu anagebainika kutaka kumsingizia mtu uongo adhabu yake ilipaswa kuwa sawa na kile alichokuwa akimshitaki mwenzi wake, waamuzi walitakiwa kuchunguza ka makini sana kama mtu anatoa ushuhuda wa uongo kisha yeye anayeshuhudia uongo alipaswa alipaswa kuhukumiwa katika kosa lileliole analolishuhudia ili mwenzake ahukumiwe

 

Kumbukumbu la torati 19:18-19 “nao waamuzi na watafute kwa bidii; na tazama, yule shahidi akiwa shahidi wa uongo, naye ametoa ushahidi wa uongo juu ya nduguye;ndipo mtamfanyia kama alivyodhani kumfanyia nduguye; ndivyo utakavyoondoa uovu katikati yako          

 

Agizo la torati liliwataka waamuzi vilevile kutokumhurumia mtu aliyewashitaki wengine kwa uongo yaani aliyetoa ushahidi wa uongo alitakiwa asihurumiwe

Kumbukumbu la torati 19:21  Wala jicho lako lisiwe na huruma; uzima kwa uzima, jicho kwa jicho, jino kwa jino, mkono kwa mkono, mguu kwa mguu.”

 

Awaye yote ambaye angemshitaki mtu kwa uongo au kutoa ushahidi wa uongo kama alikuwa ana lengo la kumuumiza mwenzake waamuzi wangebaini wangetakiwa kutokumhurumia mtu huyo na angehukumiwa sawa na kosa alilokuwa akilitolea ushaidi wa uongo bila huruma, kwa hiyo unaweza kuona kwa nini Yohana mbatizaji alikuwa mkali kwenye swala hili ni wazi kabisa ilikuwa ni kosa kubwa na zito mbele ya macho ya Mungu kushuhudia uongo dhidi ya mtu mwingine.

 

Ukiacha maamuzi yanayoweza kutolewa na waamuzi au serikali, Mungu pia huingilia kati pale askari na watu wengine wowote wanapoacha kutenda haki na kujaribu kumshitaki mtu kwa uongo, Kitabu cha Esta ni mfano uliowazi wa mtu aliyeitwa Haman ambaye alikuwa mshauri wa Mfalme Ahasuero alimshauri vibaya kwa makusudi ya kuwaangamiza wayahudi, hususani kwa sababu ya chuki yake dhidi ya Mordekai, hii ikitokana na wivu mkubwa aliokuwa nao dhidi yake unaweza kuona

 

Esta 5:9-14 “Basi Hamani alitoka siku ile kwa furaha na ukunjufu wa moyo; lakini Hamani alipomwona Mordekai mlangoni pa mfalme, ya kwamba hasimami wala kutetemeka mbele yake, alijaa ghadhabu juu ya Mordekai. Walakini Hamani akajizuia, akaenda zake nyumbani kwake; akatuma kuwaita rafiki zake na Zereshi mkewe. Naye Hamani akawasimulia habari za fahari ya mali zake, na wingi wa watoto wake, nayo mambo yote pia ambayo mfalme amemfanikisha katika hayo, na jinsi alivyompandisha juu ya maakida na watumishi wa mfalme. Zaidi ya hayo Hamani akasema, Naye malkia Esta hakumkaribisha mtu ye yote pamoja na mfalme katika karamu aliyoiandaa, ila mimi peke yangu; hata na kesho pia nimealikwa naye pamoja na mfalme. Bali haya yote yanifaa nini, pindi nimwonapo yule Mordekai, Myahudi, ameketi mlangoni pa mfalme? Basi Zereshi mkewe akamwambia, na rafiki zake wote, Na ufanyizwe mti wa mikono hamsini urefu wake, na kesho asubuhi useme na mfalme ili Mordekai atundikwe juu yake; ndipo utakapoingia kwa kicheko pamoja na mfalme karamuni. Basi neno likampendeza Hamani, akaufanyiza ule mti.” Unaweza kuona pia.

 

Esta 6:4 “Mfalme akasema, Yupo nani behewani? Ikawa Hamani alikuwa ameingia katika ua wa nje wa nyumba ya mfalme, aseme na mfalme, ili kumtundika Mordekai juu ya mti ule aliomwekea tayari.”

 

Esta 7:9-10 “Ndipo aliposema Harbona, msimamizi-wa-nyumba mmojawapo wa wale waliohudhuria mbele ya mfalme, Tazama, basi, mti wa mikono hamsini urefu wake, Hamani aliomwekea tayari Mordekai, ambaye alinena vema kwa ajili ya mfalme, upo umesimamishwa nyumbani kwa Hamani. Mfalme akasema, Mtundikeni juu yake.Basi wakamtundika Hamani juu ya mti aliomwekea tayari Mordekai. Ghadhabu ya mfalme ikatulia.”

 

Maandiko yanaonya kuwa wote wanaoshitaki wengine kwa uongo wako chini ya hukumu ya Mungu na hukumu ileile wanayoikusudia kwa wenzao itawapata wenyewe, wale waliomshitaki Daniel ili atupwe kwenye tundu la simba walitafunwa wao, maandiko yanasema kila aliyechimba shimo aliingia mwenyewe pia, Mungu hafuirahii udhalimu hata kidogo

 

Zaburi 5:4-6 “Maana huwi Mungu apendezwaye na ubaya; Mtu mwovu hatakaa kwako; Wajivunao hawatasimama mbele za macho yako; Unawachukia wote watendao ubatili. Utawaharibu wasemao uongo; Bwana humzira mwuaji na mwenye hila

 

Jambo la kushangaza ni kuwa wakati mwingine unaweza kuona kuwa hata makanisani na sehemu zenye watu wanaodhaniwa kuwa watu wa Mungu watu husingiziana, hubambikiziana kesi za uongo na kusababisha madhara makubwa wakati mwingine unaweza kuumizwa na watu wanaoshuhudia uongo lakini Mungu anajua na atakufariji kwa namna yake, Yesu alitambua kuwa wako watu wanashitakiwa kwa kubambikiziwa kwa uongo kwa kutokusimama katika haki au kuisimamia kweli

 

Mathayo 5:11-12 “Heri ninyi watakapowashutumu na kuwaudhi na kuwanenea kila neno baya kwa uongo, kwa ajili yangu. Furahini, na kushangilia; kwa kuwa thawabu yenu ni kubwa mbinguni; kwa maana ndivyo walivyowaudhi manabii waliokuwa kabla yenu”.

 

Haijalishi watu watatuzushia nini kwa uongo tumtegemee Mungu, Mungu atatulipia tu unaweza kuzushiwa uongo na kubambikiziwa kesi mbaya sana na ukaumia na kupata hasara lakini Mungu atakuja kufanya kitu

 

Zaburi 119:69-72 “Wenye kiburi wamenizulia uongo, Kwa moyo wangu wote nitayashika mausia yako. Mioyo yao imenenepa kama shahamu, Mimi nimeifurahia sheria yako. Ilikuwa vema kwangu kuwa naliteswa, Nipate kujifunza amri zako. Sheria ya kinywa chako ni njema kwangu, Kuliko maelfu ya dhahabu na fedha.”

 

Ni jambo la kusikitisha sana kuona jamii ikiwa imejaa watu ambao wanaweza kutunga jambo zito na gumu dhidi ya watu wengine na kuwaharibia maisha, wahubiri wa haki ya Mungu kama ilivyo kwa Yohana mbatizaji, asingeweza kuvumilia dhuluma katika jamii wala asingetaka Yesu Kristo aikute dhuluma lakini kutokana na jamii iliyokuwa imejaa uovu hata Yesu mwenyewe alishitakiwa kwa uongo na mafarisayo na Yesu Kristo aliposhutumiwa uongo alinyamaza kimya wala hakujibu neno

 

Isaya 53:7-8 “Alionewa, lakini alinyenyekea, Wala hakufunua kinywa chake; Kama mwana-kondoo apelekwaye machinjoni, Na kama vile kondoo anyamazavyo Mbele yao wakatao manyoya yake; Naam, hakufunua kinywa chake. Kwa kuonewa na kuhukumiwa aliondolewa; Na maisha yake ni nani atakayeisimulia? Maana amekatiliwa mbali na nchi ya walio hai; Alipigwa kwa sababu ya makosa ya watu wangu.” 

 

Unajua kwanini Yesu hakufunua kinywa chake kujitetea dhidi ya washitaki wake, maandiko yalionyesha katika Torati kuwa ni jukumu la Waamuzi kuamua na kuchunguza kwa makini kama mtu analeta ushahidi wa uongo na ni jambo la kusikitisha kuwa Pilato pia alishindwa kufanya maamuzi ya hali na kuachilia Yesu auawe huku ushahidi ukiwa wazi kuwa ni ushahidi wa uongo

 

Mathayo 27:22-26 “Pilato akawaambia, Basi, nimtendeje Yesu aitwaye Kristo? Wakasema wote, Asulibiwe. Akasema, Kwani? Ni ubaya gani alioutenda? Wakazidi sana kupiga kelele, wakisema, Na asulibiwe. Basi Pilato alipoona ya kuwa hafai lo lote, bali ghasia inazidi tu, akatwaa maji, akanawa mikono yake mbele ya mkutano, akasema, Mimi sina hatia katika damu ya mtu huyu mwenye haki; yaangalieni haya ninyi wenyewe. Watu wote wakajibu wakasema, Damu yake na iwe juu yetu, na juu ya watoto wetu. Ndipo akawafungulia Baraba; na baada ya kumpiga Yesu mijeledi, akamtoa ili asulibiwe.”             

 

Kama unadhani kubambikizia mtu kesi na kumshitaki mtu kwa uongo ni jambo jepesi ni lazima ujiohoji na uhoji kuwa ukiacha kusudi la Mungu la mwokozi kufa pale msalabani kesi ya kubambikiziwa Yesu ilimwachaje Mariamu mama yake? Na je ndugu zake Yesu na wanafunzi wake hii maana yake wale wote waliomshitaki Yesu kwa uongo nao vilevile kwa sharia ya Musa walitakiwa kusulubiwa lakini Yesu alitangaza sharia mpya ya msamaha ndio maana akawaombea baba uwasamehe kwa maana hawajui walitendalo ni kwaajili ya haya mahubiri ya Yihana mbatizaji na makatazo yake yalikuwa ni ya muhimu sana kwa wanadamu na jamii sio tu ya wakati ule bali hata naya wakati wa sasa.

 

3.       Kutokutosheka na Mishahara –

 

Yohana aidha aliwajibu na kuwataka askari vilevile kutosheka na mishahara yao, ni wazi kuwa kutokuridhika ni tatizo kubwa sana la mwanadamu tangu anguko la mwanadamu lilipotokea hakuna kitu kinatosha wanadamu wamekuwa na tamaa na miongoni mwao wakiwa askari kwa sababu wao kama walinda usalama katika jamii wana nafasi ya kuona fursa mbalimbali na hivyo ni rahisi kwao kama ilivyo vilevile kwa watu wengine kuingia katika mlango wa tamaa hususani katika fedha na kuwa na roho ya kutokutosheka

 

1Timotheo 6:7-10  Kwa maana hatukuja na kitu duniani, tena hatuwezi kutoka na kitu; ila tukiwa na chakula na nguo tutaridhika na vitu hivyo. Lakini hao watakao kuwa na mali huanguka katika majaribu na tanzi, na tamaa nyingi zisizo na maana, zenye kudhuru, ziwatosazo wanadamu katika upotevu na uharibifu. Maana shina moja la mabaya ya kila namna ni kupenda fedha; ambayo wengine hali wakiitamani hiyo wamefarakana na Imani, na kujichoma kwa maumivu mengi.”

 

Hali ya kutokuridhika na kuwa na tamaa kwa vyombo ambavyo vinatakiwa kuwa mstari wa mbele katika kutoa haki au kwa mwanadamu awaye yote ni tatizo la siku nyingi katika jamii mbalimbali hali hii huharibu uhusiano wetu na Mungu na wanadamu na kuharibu hali ya kiroho, Mungu angehukumu vilevile hali hii kwani hata zamani katika Israel ilikuwa ni njia ya matajiri kujipatia utajiri kwa njia zilizoharamu maswala haya yalikemewa na manabii kama Amosi, Mika na Yeremia Mfano katika kitabu cha Amos watu waliweza kuuza utu wa watu kwa sababu ya jozi za viatu tu 

 

Amosi 2:6b “Haya ndiyo asemayo Bwana; Kwa makosa matatu ya Israeli, naam, kwa manne, sitaizuia adhabu yake isimpate; kwa sababu wamewauza wenye haki kwa fedha, na maskini kwa jozi ya viatu;”

 

Kwa msingi huo Yohana katika mahubiri yake alikuwa akiitaka jamii hususani askari kuwa na shukrani kuridhika kwani moja ya matunda ya ukomavu wa ubinadamu ni pamoja na kuridhika Lakini Mungu anawataka watu wake kuitenda haki ili Baraka za Mungu ziweze kumiminika katika maisha yetu

 

Mika 6:8 “Ee mwanadamu, yeye amekuonyesha yaliyo mema; na Bwana anataka nini kwako, ila kutenda haki, na kupenda rehema, na kwenda kwa unyenyekevu na Mungu wako!

Lazima jamii ikubaliane na maandiko kuwa unapaswa ufike wakati turidhike na maandiko yanatufundisha kuwa kuridhika kuna faida kubwa sana

 
1Timotheo 6:6-19 “Walakini utauwa pamoja na kuridhika ni faida kubwa. Kwa maana hatukuja na kitu duniani, tena hatuwezi kutoka na kitu; ila tukiwa na chakula na nguo tutaridhika na vitu hivyo. Lakini hao watakao kuwa na mali huanguka katika majaribu na tanzi, na tamaa nyingi zisizo na maana, zenye kudhuru, ziwatosazo wanadamu katika upotevu na uharibifu. Maana shina moja la mabaya ya kila namna ni kupenda fedha; ambayo wengine hali wakiitamani hiyo wamefarakana na Imani, na kujichoma kwa maumivu mengi. Bali wewe, mtu wa Mungu, uyakimbie mambo hayo; ukafuate haki, utauwa, imani, upendo, saburi, upole. Piga vita vile vizuri vya imani; shika uzima ule wa milele ulioitiwa, ukaungama maungamo mazuri mbele ya mashahidi wengi. Nakuagiza mbele za Mungu anayevihifadhi hai vitu vyote, na mbele za Kristo Yesu, aliyeyaungama maungamo mazuri yale mbele ya Pontio Pilato, kwamba uilinde amri hii pasipo mawaa, pasipo lawama, hata kufunuliwa kwake Bwana wetu Yesu Kristo; ambako yeye kwa majira yake atakudhihirisha, yeye aliyehimidiwa, Mwenye uweza peke yake, Mfalme wa wafalme, Bwana wa mabwana; ambaye yeye peke yake hapatikani na mauti, amekaa katika nuru isiyoweza kukaribiwa; wala hakuna mwanadamu aliyemwona, wala awezaye kumwona. Heshima na uweza una yeye hata milele. Amina.Walio matajiri wa ulimwengu wa sasa uwaagize wasijivune, wala wasiutumainie utajiri usio yakini, bali wamtumaini Mungu atupaye vitu vyote kwa wingi ili tuvitumie kwa furaha. Watende mema, wawe matajiri kwa kutenda mema, wawe tayari kutoa mali zao, washirikiane na wengine kwa moyo; huku wakijiwekea akiba iwe msingi mzuri kwa wakati ujao, ili wapate uzima ulio kweli kweli

 

Kwa mtindo huu utakubaliana nami kuwa Nabii Yohana mbatizaji alikuwa Mtu aliyeibhubiri haki ya Mungu kwa konyooka bila kujali cheo cha mtu yeye aliwaonya watu wote masikini kwa matajiri, wafalme na hata watumwa akiwataka wote kuandaa njia ya masihi na kuwa tayari kwa mioyo iliyotubu mbele za Mungu.kila mmoja  hana budi kujiuliza nay eye je anafanya nini katika nafasui yake! Na afanye ulio wajibu wake

 

Na Rev. Innocent Kamote

Mkuu wa wajenzi mwenye hekima

Hakuna maoni: