Ijumaa, 15 Aprili 2022

Baba uwasamehe, kwa kuwa hawajui watendalo!


Luka 23:33-37 “Na walipofika mahali paitwapo Fuvu la Kichwa, ndipo walipomsulibisha yeye, na wale wahalifu, mmoja upande wa kuume, na mmoja upande wa kushoto. Yesu akasema, BABA, UWASAMEHE, KWA KUWA HAWAJUI WATENDALO. Wakagawa mavazi yake, wakipiga kura. Watu wakasimama wakitazama. Wale wakuu nao walikuwa wakimfanyia mzaha, wakisema, Aliokoa wengine; na ajiokoe mwenyewe, kama ndiye Kristo wa Mungu, mteule wake. Wale askari nao wakamfanyia dhihaka, wakimwendea na kumletea siki, huku wakisema, Kama wewe ndiwe mfalme wa Wayahudi, ujiokoe mwenyewe



Utangulizi:


Mojawapo kati ya usemi wenye maana sana kati ya semi saba za Yesu alizozisema akiwa msalabani na ambazo zinatajwa katika sehemu mbalimbali za injili, ni pamoja ya usemi huo wa muhimu ni usemi wa Kwanza wenye Neno BABA UWASAMEHE KWA MAANA HAWAJUI WALITENDALO ambalo leo katika msimu huu wa pasaka tutachukua muda kulijadili kwa undani na kupata maana Muhimu sana iliyokusudiwa, maneno mengine kati ya maneno saba aliyoyasema Yesu msalabani ni pamoja na:-

1.       Baba uwasamehe kwa maana hawajui walitendalo Luka 23:34

2.       Amin nakuambia leo hii utakuwa pamoja nani peponi Luka 23:43

3.       Mama tazama mwanao, mwana tazama mama yako Yohana 19:26-27

4.       Mungu wangu Mungu wangu mbona umeniacha Mathayo 27:46

5.       Nina kiu Yohana 19:28

6.       Imekwisha Yohana 19:30

7.       Baba mikononi mwako naiweka roho yangu Luka 23:46



BABA UWASAMEHE KWA MAANA HAWAJUI WALITENDALO.


Leo ni siku ya ijumaa kuu, ni siku ambayo wakristo wote duniani, tunaungana katika kuadhimisha na kukumbuka kusulubiwa kwa Yesu Kristo huko Golgota miaka zaidi ya 2000 iliyopita katika siku hii basi basi sisi tutachukua Muda kuangalia usemi huu wa Kwanza katika maneno saba yaliyozungumzwa na Yesu Pale Msalabani wakati wa mateso yake , Neno hili ni miongoni mwa maneno saba ya Yesu akiwa matesoni ambayo yamekusanywa kutoka maeneo mbalimbali ya vitabu vya injili na hili mojawapo tutaangalia umuhimu wake katika msimu huu wa Pasaka. Hapa tunazungumzia Msamaha.


Kila mmoja wetu kwa namna moja ama nyingine amewahi kujeruhiwa moyo na mtu mwingine, kila mmoja amewahi kujeruhiwa na kuathiriwa kiakili, kihisia na hata kimwili, na kwa sababu hiyo tunaweza kujawa na maumivu ya aina Fulani mioyoni mwetu, ama uchungu wa aina Fulani, vyovyote vile iwavyo ukomavu wa kiroho katika maisha yetu ya ukristo unapimwa na namna tunavyoweza kusamehe, uwezo wa kusamehe ukiwa pamoja nasi  unatuwezesha kuishi kwa furaha na amani duniani na huku tukiwa huru bila kifungo chochote endapo tutakuwa na uwezo wa kusamehe wengine.


Yesu Kristo akiwa Msalabani aliangalia chini na kutafakari katika hali ya ukimya akiwaangalia wote waliokuwa wanahusika katika kumtesa, Askari ambao walisimamia mateso yake wakigawana nguo yake kwa kuipigia kura, Yesu hakuwahi kutenda neno lolote ovu, siku zote alikuwa akiwafundisha watu neno la Mungu na kuwaponya watu magonjwa yao, aliwahudumia watu akifufua, akiponya, akilisha akihurumia na kurehemu, hata hivyo kwajili ya wivu wakuu wa dini walikusudia kumuua, waliandaa mpango mkakati wa kumuua, walitoa rushwa kwa Yuda ili aweze kumsaliti, waliandaa mashahidi wa uongo ili wamshitaki, walimuweka katima mikono ya wenye dhambi ili asulubiwe, hakimu aliyekuwepo alipindisha hukumu ilihali akijua wazi kuwa Yesu hakuwa na hatia, zaidi ya yote aliamuru Yesu apigwe mijeledi 


Yohana 19:1-6 “Basi ndipo Pilato alipomtwaa Yesu, akampiga mijeledi. Nao askari wakasokota taji ya miiba, wakamtia kichwani, wakamvika vazi la zambarau. Wakawa wakimwendea, wakisema, Salamu! Mfalme wa Wayahudi! Wakampiga makofi. Kisha Pilato akatokea tena nje, akawaambia, Mtu huyu namleta nje kwenu, mpate kufahamu ya kuwa mimi sioni hatia yo yote kwake. Ndipo Yesu alipotoka nje, naye amevaa ile taji ya miiba, na lile vazi la zambarau. Pilato akawaambia, Tazama, mtu huyu! Basi wale wakuu wa makuhani na watumishi wao walipomwona, walipiga kelele wakisema, Msulibishe! Msulibishe! Pilato akawaambia, Mtwaeni ninyi basi, mkamsulibishe; kwa maana mimi sioni hatia kwake.”


Ni ukweli usiopingika kuwa Yesu aliharibiwa sana kiasi ambacho ilikuwa ni ngumu kumtamani sawa kabisa na alivyotabiri Isaya katika Isaya 53:2-5Maana alikua mbele zake kama mche mwororo, Na kama mzizi katika nchi kavu; Yeye hana umbo wala uzuri; Na tumwonapo hana uzuri hata tumtamani. Alidharauliwa na kukataliwa na watu; Mtu wa huzuni nyingi, ajuaye sikitiko; Na kama mtu ambaye watu humficha nyuso zao, Alidharauliwa wala hatukumhesabu kuwa kitu. Hakika ameyachukua masikitiko yetu, Amejitwika huzuni zetu; Lakini tulimdhania ya kuwa amepigwa, Amepigwa na Mungu, na kuteswa. Bali alijeruhiwa kwa makosa yetu, Alichubuliwa kwa maovu yetu; Adhabu ya amani yetu ilikuwa juu yake, Na kwa kupigwa kwake sisi tumepona.”


Pamoja na mateso haya na suluba kali pia walimfanyia dhihaka za namna nyingi, mateso yake yamerekodiwa na Mel Gobson katika filamu yake ijulikanayo kama Passion of Jesus ambayo wayahudi walipoiona kwa mara ya kwanza waliikataa na kusema kuwa inaweza kuchochea chuki kati ya wakristo na wayahudi wakifikiri kuwa Mel Gibson ametia chumvi, lakini kitaalamu Mel Gibson ameonyesha karibu robo tatu tu ya mateso halisi aliyoyapata Kristo, mateso mengine :- 


Yohana 19:23-24, “Nao askari walipomsulibisha Yesu, waliyatwaa mavazi yake, wakafanya mafungu manne, kwa kila askari fungu lake; na kanzu nayo. Basi kanzu ile haikushonwa, ilikuwa imefumwa yote pia tangu juu. Basi wakaambiana, Tusiipasue, lakini tuipigie kura, iwe ya nani. Ili litimie andiko lile linenalo, Waligawanya nguo zangu, Na vazi langu wakalipigia kura. Basi ndivyo walivyofanya wale askari.” 


Mathayo 27:27-31 “Ndipo askari wa liwali wakamchukua Yesu ndani ya Praitorio, wakamkusanyikia kikosi kizima.Wakamvua nguo, wakamvika vazi jekundu. Wakasokota taji ya miiba, wakaiweka juu ya kichwa chake, na mwanzi katika mkono wake wa kuume; wakapiga magoti mbele yake, wakamdhihaki, wakisema, Salamu, Mfalme wa Wayahudi! Kisha wakamtemea mate, wakautwaa ule mwanzi, wakampiga-piga kichwani. Walipokwisha kumdhihaki, wakalivua lile vazi, wakamvika mavazi yake, wakamchukua kumsulibisha.” 


Wahalifu wawili waliokuwa kulia kwake na kushoto kwake wakimshutumu, Mathayo 27:44, “Pia wale wanyang'anyi waliosulibiwa pamoja naye walimshutumu vile vile.” Viongozi wa dini waliofanya fitina na kutengeneza ushahidi wa uongo na kushinikiza kwamba Yesu asulubiwe na waliokuwa wakimdhihaki Mathayo 27:41-43,“Kadhalika na wale wakuu wa makuhani wakamdhihaki pamoja na waandishi na wazee, wakisema, Aliokoa wengine, hawezi kujiokoa mwenyewe. Yeye ni mfalme wa Israeli; na ashuke sasa msalabani, nasi tutamwamini. Amemtegemea Mungu; na amwokoe sasa, kama anamtaka; kwa maana alisema, Mimi ni Mwana wa Mungu” 


Hakimu Pilato ambaye alifahamu kabisa kuwa Yesu hakuwa na hatia, lakini akapindisha kesi haya yote na ile aina ya mateso kwa mwana wa Mungu, kungeweza kwa namna yoyote ile kuleta hisia za maumivu, uchungu, kinyongo, kisasi, ugumu wa moyo, hasira, ghadhabu, ubaridi, kujihami na kuhakikisha kuwa unawashughulikia wote waliokutenda uovu, Lakini Bwana Yesu anatangaza kusamehe na kuwaombea wakosaji wote kwa BABA KUWA WASAMEHEWE, Hali hii inaashiria uwezo mkubwa wa ukomavu mkubwa wa kiroho aliokuwa nao Yesu wa kutangaza Msamaha, ni ngazi ya juu sana ya Rehema na upendo, kwamba hata katika hali ngumu kama hii ya kuteseka bado Yesu anatangaza Msamaha dhidi ya maadui zake ! wote tunafahamu kuwa msamaha sio jambo rahisi, lakini katika msimu huu wa Pasaka Bwana Yesu anatukumbusha kwamba tunapaswa kuachilia na kutangaza msamaha kwa wote waliotukosea lakini vilevile kuwaomba radhi wale ambao tumewakosea, wakati huu wa Kwaresma ni wakati wa kuachilia ni wakati wa kusamehe ni wakati wa kuonyesha kuwa tumekomaa kiroho na kiakili na kuwa kusamehe ndio njia ya juu kabisa ya kuonyesha tabia ya uungu na ukomavu wetu, tusamehe.! 


Kusamehe ni nini hasa? 


Kusamehe ni kuachilia, unaachilia mambio yaende, unaacha kuhesabu ubaya uliofanyiwa unaufunika kwa kuendelea kupenda, unaacha kutafuta kulipa kisasi au nkulipiwa kisasi, unaondoa moyoni mwako hali ya kumfikiri mtu aliyekukosea unajiweka huru mbali na kifungo cha aina yoyote cha kuwa na mtu moyoni, unamuhurumia mtu, unachukuliana naye, unamuhesabu kuwa yeye ni dhaifu, hivyo unamuachilia 


Faida za kusamehe 


·         Unadumisha mahusiano, mahusiano yanakuwa mazuri, Ndoa inakuwa nzuri, unampata ndugu yako

·         Unaiweka akili yako kufikiri mambo ya msingi na kuzungumza mambo ya msingi

·         Unajiweka huru kutoka kwenye migandamizo na msongo wa mawazo

·       Unakuwa na afya nzuri, unakuwa mwenye furaha, hutakuwa na pressure, hutaugua magonjwa ya moyo, na unakuwa mtu mwenye uwezio wa juu wa kujitambua 


·         Kusamehe kunakufanya wewe nawe usamehewe na Mungu 


Mathayo 18:21-35Kisha Petro akamwendea akamwambia, Bwana, ndugu yangu anikose mara ngapi nami nimsamehe? Hata mara saba? Yesu akamwambia, Sikuambii hata mara saba, bali hata saba mara sabini. Kwa sababu hii ufalme wa mbinguni umefanana na mfalme mmoja aliyetaka kufanya hesabu na watumwa wake. Alipoanza kuifanya, aliletewa mtu mmoja awiwaye talanta elfu kumi.Naye alipokosa cha kulipa, bwana wake akaamuru auzwe, yeye na mkewe na watoto wake, na vitu vyote alivyo navyo, ikalipwe ile deni.Basi yule mtumwa akaanguka, akamsujudia akisema, Bwana, nivumilie, nami nitakulipa yote pia. Bwana wa mtumwa yule akamhurumia, akamfungua, akamsamehe ile deni. Mtumwa yule akatoka, akamwona mmoja wa wajoli wake, aliyemwia dinari mia akamkamata,akamshika koo,akisema Nilipe uwiwacho.Basi mjoli wake akaanguka miguuni pake, akamsihi, akisema, Nivumilie, nami nitakulipa yote pia. Lakini hakutaka, akaenda, akamtupa kifungoni, hata atakapoilipa ile deni. Basi wajoli wake walipoyaona yaliyotendeka, walisikitika sana, wakaenda wakamweleza bwana wao yote yaliyotendeka. Ndipo bwana wake akamwita, akamwambia, Ewe mtumwa mwovu, nalikusamehe wewe deni ile yote, uliponisihi; nawe, je! Haikukupasa kumrehemu mjoli wako, kama mimi nilivyokurehemu wewe? Bwana wake akaghadhibika, akampeleka kwa watesaji, hata atakapoilipa deni ile yote. Ndivyo na Baba yangu wa mbinguni atakavyowatenda ninyi, msiposamehe kwa mioyo yenu kila mtu ndugu yake.” 


Kutokusamehe hasara zake. 


Hakuna sababu ya kuwabeba watu moyoni, hii hali kiroho inakuweka wewe mwenyewe gerezani na kukunyima furaha, dua, sala, sadaka na maombi yetu vinakutana na kikwazo kama hatujawasamehe wengine Mathayo 6:12 “Utusamehe deni zetu, kama sisi nasi tuwasamehevyo wadeni wetu.” Mathayo 6:14-15 “Kwa maana mkiwasamehe watu makosa yao, na Baba yenu wa mbinguni atawasamehe ninyi.Bali msipowasamehe watu makosa yao, wala Baba yenu hatawasamehe ninyi makosa yenukuna hasara nyingi sana za kiroho na kimwili kama watu hawatasamehe na kuna faida nyingi sana kama watu watasamehe.Lakini kama mtu hatasamehe yafuatayo yatamkabili:- 


·         Unakuwa na moyo wenye uchungu, huwezi kufurahia mahusiano hata katika ndoa

·         Unakuwa na mawazo mabaya kwa kudhani Fulani ni adui yako

·         Utakuwa na mgandamizo wa mawazo

·         Unafungua mlango wa kuvamiwa na mapepo, unafukuza uwepo wa Mungu

·         Unazuia Baraka za Mungu na kufanya ibada zako zikataliwe

Bwana na ampe neema kila Mmoja wetu, kuwa na uwezo wa kusamehe ili tuweze kuwa wana wa Mungu sawasawa na mafundisho ya Bwana wetu Yesu!

 

Na. Rev. Innocent Kamote

Mkuu wa wajenzi mwenye Hekima



Hakuna maoni: