Jumapili, 24 Desemba 2023

Tuliiona Nyota yake!


Mathayo 2:1-12Yesu alipozaliwa katika Bethlehemu ya Uyahudi zamani za mfalme Herode, tazama, mamajusi wa mashariki walifika Yerusalemu, wakisema, Yuko wapi yeye aliyezaliwa mfalme wa Wayahudi? Kwa maana tuliiona nyota yake mashariki, nasi tumekuja kumsujudia.”




Utangulizi:

Moja ya stori zenye mvuto mkubwa sana katika Biblia ni pamoja na stori ya ujio wa watu wenye hekima kutoka mashariki ya mbali waliokuja kutoka Mashariki ya mbali wakiongozwa na nyota mpaka Bethelehemu alikozaliwa Masihi, kwaajili ya kumuabudu, Stori hii Mathayo ameipa uzito mkubwa sana na maneno yao yenye mvuto mkubwa zaidi ni haya:- Yuko wapi yeye aliyezaliwa mfalme wa Wayahudi? Kwa maana tuliiona nyota yake mashariki, nasi tumekuja kumsujudia. Utamu wa maneno yao na matendo yao unanifanya leo nitulie na kutafakari pamoja nawe jambo kubwa ambalo Mungu amelifanya kupitia wenye hekima hao maarufu kama mamajusi kwa Kiswahili cha zamani, (kwa sasa wenye hekima- Wise man); Leo tutachukua muda kujifunza kwa kina na mapana na marefu kuhusiana na swala hili:-

Ufahamu kuhusu Mamajusi.

Mojawapo ya tukio maarufu na la kusisimua sana wakati inapokaribia sikukuu ya Krismasi ni pamoja na safari ya ujio wa Mamajusi kutoka mashariki, Kimsingi neno mamajusi kwa kiingereza “Magi” linatokana na neno la kiyunani MAGOS ambalo ni sawa na neno Magician ambao zamani walijumuishwa katika kundi la watu wenye hekima, wachawi na wanajimu waliokuwa na sayansi ya kutoa suluhu kunapotokea changamoto katika falme za Babeli  angalia kwa mfano katika kitabu cha Daniel

Daniel 2:1-3 “Hata katika mwaka wa pili wa kumiliki kwake Nebukadreza, Nebukadreza aliota ndoto; na roho yake ikafadhaika, usingizi wake ukamwacha. Ndipo mfalme akatoa amri kuwaita waganga, na wachawi, na wasihiri, na Wakaldayo, wapate kumweleza mfalme ndoto zake. Basi wakaingia, wakasimama mbele ya mfalme. Mfalme akawaambia, Nimeota ndoto, na roho yangu imefadhaika hata niijue tafsiri yake.”

Daniel 5:4-9. “Wakanywa divai, wakaisifu miungu ya dhahabu, na ya fedha, na ya shaba, na ya chuma, na ya mti, na ya mawe. Saa iyo hiyo vikatokea vidole vya mkono wa mwanadamu, vikaandika katika chokaa ya ukuta wa nyumba ya enzi ya mfalme, mahali palipokikabili kinara; naye mfalme akakiona kitanga cha ule mkono ulioandika. Ndipo uso wa mfalme ukambadilika; fikira zake zikamfadhaisha; viungo vya viuno vyake vikalegea; magoti yake yakagongana. Mfalme akalia kwa sauti kubwa, akaamuru waletwe wachawi, na Wakaldayo na wanajimu. Mfalme akanena, akawaambia wenye hekima wa Babeli, mtu awaye yote atakayesoma maandiko haya, na kunionyesha tafsiri yake, atavikwa mavazi ya rangi ya zambarau, na kuwa na mkufu wa dhahabu shingoni mwake, naye atakuwa mtu wa tatu katika ufalme. Basi wakaingia wenye hekima wote wa mfalme; lakini hawakuweza kuyasoma yale maandiko, wala kumjulisha mfalme tafsiri yake. Ndipo mfalme Belshaza akahangaika sana, uso wake ukambadilika, na wakuu wake wakaona fadhaa.”

Kwa hiyo ilikuwa kawaida ya wafalme wa zamani walipopata changamoto za aina mbalimbali katika falme zao kuwaita wenye hekima (Wiseman) ili waweze kutatua changamoto mbalimbali walizokuwa wanakutana nazo hawa ndio waliitwa MAGI au Mamajusi au wenye hekima, kwa kusudi la kutatua changamoto zao

Tukio linalofanana na hayo hapo juu lilitokea mapema zaidi ya miaka 1000 kabla ya kuzaliwa kwa Yesu, wakati wana wa Israel walipokuwa wakitokea Misri na kuwapiga wafalme wa waamori, mfalme wa Moabu aliogopa sana na hivyo alimuita mchawi aliyeitwa Balaam ili aje kuwaroga au kuwalaani Israel wasiweze kumdhuru

Hesabu 22:1-6 “Kisha wana wa Israeli wakasafiri na kupanga katika nchi tambarare za Moabu ng'ambo ya pili ya Yordani karibu ya Yeriko. Na Balaki mwana wa Sipori akaona mambo yote ambayo Israeli wamewatendea Waamori. Moabu akawaogopa hao watu sana, kwa kuwa walikuwa wengi; Moabu akafadhaika kwa sababu ya wana wa Israeli. Moabu akawaambia wazee wa Midiani, Sasa jeshi hili la watu litaramba vitu vyote vinavyotuzunguka, kama vile ng'ombe arambavyo majani ya mashamba. Na Balaki, mwana wa Sipori, alikuwa mfalme wa Moabu zamani zile. Basi akatuma wajumbe kwa Balaamu mwana wa Beori, hata Pethori, ulio kando ya Mto, mpaka nchi ya wana wa watu wake, kwenda kumwita, akisema, Tazama, kuna watu waliotoka Misri; tazama, wanaufunika uso wa nchi, tena wanakaa kunikabili mimi. Basi, njoo wewe, nakusihi unilaanie watu hawa; maana wana nguvu kunishinda mimi. Labda nitawaweza, tupate kuwapiga, niwafukuze watoke katika nchi yangu, kwa maana najua ya kuwa yeye umbarikiye hubarikiwa, na yeye umlaaniye hulaaniwa.”

Hata hivyo katika namna ya kushangaza Nabii huyu badala ya kuwalaani Israel yeye aliwabariki sawa na jinsi Mungu alivyomuamuru, Ujumbe wa Mungu kwa Balaki kupitia Balaamu ulikuwa na maonyo makubwa sana badala ya kulaani aliamuriwa kuibariki Israel na kutoa unabii kuwa atakuja mfalme mwenye nguvu sana na Mfalme huyo atawahukumu maadui wa Israel mfalme huyo mkuu ilionekana nyota yake alisema namwona lakini si sasa Namtazama lakini si karibu Nyota itatokea Katika Israel:-  

Hesabu 24:15-19 “Akatunga mithali yake akasema, Balaamu mwana wa Beori asema, Yule mtu aliyefumbwa macho asema, Asema, yeye asikiaye maneno ya Mungu, Na kuyajua maarifa yake Aliye Juu. Yeye aonaye maono ya Mwenyezi, Akianguka kifudifudi, amefumbuliwa macho, Namwona, lakini si sasa; Namtazama, lakini si karibu; Nyota itatokea katika Yakobo Na fimbo ya enzi itainuka katika Israeli; Nayo itazipiga-piga pembe za Moabu, Na kuwavunja-vunja wana wote wa ghasia. Na Edomu itakuwa milki Seiri pia itakuwa milki, waliokuwa adui zake; Israeli watakapotenda kwa ushujaa. Mwenye kutawala atakuja toka Yakobo, Atawaangamiza watakaobaki mjini.”

Unabii huo kimsingi ulikuwa unamuhusu Daudi katika mawazo finyu na unamuhusu Yesu Kristo katika mawazo mapana, (in a narrow sense, Daivid, in a broad Sense Jesus)  Huenda unabii huu ulihifadhiwa na wanajimu wa ukaldayo, ama ulisomwa nao katika vitabu vya kale, ama walisoma kitabu cha Daniel na kuwa na ufahamu wa Muda kamili wa kuja kwa mfalme huyu mkuu sana wa wayahudi

Daniel 9:24-25 “Muda wa majuma sabini umeamriwa juu ya watu wako, na juu ya mji wako mtakatifu, ili kukomesha makosa, na kuishiliza dhambi, na kufanya upatanisho kwa ajili ya uovu, na kuleta haki ya milele, na kutia muhuri maono na unabii, na kumtia mafuta yeye aliye mtakatifu. Basi ujue na kufahamu, ya kuwa tangu kuwekwa amri ya kutengeneza na kuujenga upya Yerusalemu hata zamani zake MASIHI ALIYE MKUU; kutakuwa na majuma saba; na katika majuma sitini na mawili utajengwa tena pamoja na njia kuu zake na handaki, naam, katika nyakati za taabu.”                

Na au mara katika sayansi yao ya unajimu walipoiona nyota  ambao kwa kusema kweli walikuwa na uelewa wa moja kwa moja kuwa kiongozi huyo ni Mfalme mkuu wa ulimwengu mzima na anayepaswa kuabudiwa,

Katika kundi la wenye Hekima kulikuwa na wanajimu ambao nao walikuwa wakifanya kazi katika jumba la kifalme kazi yao kubwa ni kuwa waliamini katika mwendo wa nyota na walikuwa na uwezo wa kutambua kila jambo muhimu linalotokea duniani kupitia nyota, kwa hiyo ilikuwa ni kazi yao kutoa taarifa kwa mfalme endapo kuna jambo lolote Muhimu limetokea Duniani, waliamini kuwa mwenendo wa nyota unaashiria tukio Fulani duniani kwa hiyo ilikuwa ni kazi yao kuzisoma na kuzichunguza angani wakati wa usiku ili kutambua jambo muhimu linalotokea duniani na wakisha kugundua walimpa taarifa mfalme kuhusu taarifa walizozibaini.

Katika tukio hili wenye hekima hawa waliongozwa na nyota hii ambayo ilikuwa ikimwakilisha masihi ni kwaajili ya hayo sasa unaweza kuona Mathayo analichukua tukio la ujio wa mamajusi kama mojawapo ya tukio la kimuujiza linalomuonyesha Yesu kuwa ni Mfalme wa wayahudi na ni mfalme wa ulimwengu na kuwa amekuja kwaajili ya watu wote,

Mathayo 2:1-2 “Yesu alipozaliwa katika Bethlehemu ya Uyahudi zamani za mfalme Herode, tazama, mamajusi wa mashariki walifika Yerusalemu, wakisema, Yuko wapi yeye aliyezaliwa mfalme wa Wayahudi? Kwa maana tuliiona nyota yake mashariki, nasi tumekuja kumsujudia.”

Mamajusi walikuwa na utambuzi kupitia nyota waliyoiona kuwa ilikuwa inaashiria kwamba amezaliwa Mfalme na kiongozi mkuu sana swa na unabii wa Kiyahudi, baadaye Nyota hiyo iliwaongoza mpaka Bethelehemu mahali ambapo kweli walimkuta Mtoto huyo ambaye ni Bwana wetu Yesu Kristo, walijawa na furaha kubwa sana na walimuabudu na kutoa sadaka yao

Mathayo 2:8-12. “Akawapeleka Bethlehemu, akasema, Shikeni njia, mkaulize sana mambo ya mtoto; na mkiisha kumwona, nileteeni habari, ili mimi nami niende nimsujudie. Nao waliposikia maneno ya mfalme, walishika njia; na tazama, ile nyota waliyoiona mashariki ikawatangulia, hata ikaenda ikasimama juu ya mahali alipokuwapo mtoto. Nao walipoiona ile nyota, walifurahi furaha kubwa mno. Wakaingia nyumbani, wakamwona mtoto pamoja na Mariamu mamaye, wakaanguka wakamsujudia; nao walipokwisha kufungua hazina zao, wakamtolea tunu; dhahabu na uvumba na manemane. Nao wakiisha kuonywa na Mungu katika ndoto wasimrudie Herode, wakaenda zao kwao kwa njia nyingine.”

Kinyume na furaha waliyokuwanayo mamajusi Mfalme Herode yeye hakuwa na furaha, badala yake aliwaita mamajusi na kutaka kujua muda sahihi tangu walipoiona ile nyota akidai kwamba ili na yeye aweze kwenda kumshujudia, hata hivyo akiwa na nia ovu na mpango wa siri wa kumuua mtoto Yesu

Mathayo 2:3-8 “Basi mfalme Herode aliposikia hayo, alifadhaika, na Yerusalemu pia pamoja naye. Akakusanya wakuu wa makuhani wote na waandishi wa watu, akatafuta habari kwao, Kristo azaliwa wapi? Nao wakamwambia, Katika Bethlehemu ya Uyahudi; kwa maana ndivyo ilivyoandikwa na nabii, Nawe Bethlehemu, katika nchi ya Yuda, Hu mdogo kamwe katika majumbe wa Yuda; Kwa kuwa kwako atatoka mtawala Atakayewachunga watu wangu Israeli. Kisha Herode akawaita wale mamajusi faraghani, akapata kwao hakika ya muda tangu ilipoonekana ile nyota. Akawapeleka Bethlehemu, akasema, Shikeni njia, mkaulize sana mambo ya mtoto; na mkiisha kumwona, nileteeni habari, ili mimi nami niende nimsujudie

Ashukuriwe Mungu kwa sababu alifahamu nia ya Herode na hivyo Mungu alisema na mamajusi na kuwaonya kutokurudi Yerusalem na kumpa taarifa mfalme kwani alikuwa na nia ovu,

Mathayo 2:1-13 “Nao wakiisha kuonywa na Mungu katika ndoto wasimrudie Herode, wakaenda zao kwao kwa njia nyingine. Na hao walipokwisha kwenda zao, tazama, malaika wa Bwana alimtokea Yusufu katika ndoto, akasema, Ondoka, umchukue mtoto na mama yake, ukimbilie Misri, ukae huko hata nikuambie; kwa maana Herode anataka kumtafuta mtoto amwangamize.”

Tukio hili linatufundisha ya kuwa Mungu ni mwenye nguvu kubwa sana na ndiye anayeutawala ulimwengu na vyote vilivyomo, yeye hufanya kazi katika mazingitra yoyote kutokezesha kile ambacho yeye anakitaka, anaweza kufanya chochote kwa kawaida au kwa njia ya muujiza, anaweza kuingilia kati lolote kwa yoyote kwa jinsi yoyote, Mungu yuko nyuma ya kila tukio linalotokea Duniani, Hakuna sababu ya kulaumu chochote wala kujisumbua kwa lolote linalotutokea Duniani wala hatupaswi kumuhoji Mungu kwanini hili linatokea, Mungu anajua kila kitu ana nguvu ya kutumia mazingira na ana nguvu ya kuwatumia watu wote, anauwezo wa kuzungumza hata na wanajimu, na wachawi na waganga na wenye hekima na hakuna mtu wa kukutikisa wala kubadilisha makusudi na mpango wa Mungu katika maisha yako na yangu!

Herode ambaye ni adui mkubwa wa Yesu Kristo aliweza kutambua kuwa Yesu ni nani na alimuogopa, alifahamu kuwa Yesu ndiye mtawala wa ulimwengu na ni mfalme mwenye nguvu na kuwa kila kitu katika maisha yake kinatakiwa kubadilika na hivyo alikusudia kumuua.

Dunia haiwezi kuvumilia kujua na kuona nyota yako iking’ara, hawawezi kufurahia mafanikio yako, unapoona unapigwa vita kubwa maana yake umebeba kusudi kubwa, vita kubwa kazi kubwa, mtu mkubwa majaribu makubwa, mtu mgumu majaribu magumu lakini yote katika yote Mungu anachukua utawala anamiliki kila jambo, Mungu ndiye mratibu wa kila jambo kwenye maisha yetu na hivyo hatupaswi kuogopa, kama alivyo mtetea mwanaye atatutetea na sisi, kama alivyomficha mwanae kule Misri atakuficha na wewe hata watakapoangamia wote wanaoitafuta roho yako, unapokaribia kuiadhimisha siku njema ya Christmas na kuadhimisha kuzaliwa kwake kumbuka yeye ni mtetezi wetu aliye hai na atakwenda kukutetea ni wakati wa nyota yako kung’aa na hakuna wa kukuzuia uwe na wakati mzuri na mkesha mzuri wa kuadhimisha kuzaliwa kwa Kirsto katika jina la Yesu Kristo ameen!

Zaburi 46:1-3 “Mungu kwetu sisi ni kimbilio na nguvu, Msaada utakaoonekana tele wakati wa mateso. Kwa hiyo hatutaogopa ijapobadilika nchi, Ijapotetemeka milima moyoni mwa bahari. Maji yake yajapovuma na kuumuka, Ijapopepesuka milima kwa kiburi chake.”

Rev. Innocent Samuel Kamote

Mkuu wa Wajenzi mwenye Hekima!

Hakuna maoni: