Jumatano, 6 Desemba 2023

Kutumia kwa Halali neno la kweli


2Timotheo 2:15-18 “Jitahidi kujionyesha kuwa umekubaliwa na Mungu, mtenda kazi asiye na sababu ya kutahayari, ukitumia kwa halali neno la kweli. Jiepushe na maneno yasiyo na maana, ambayo si ya dini; kwa kuwa wataendelea zaidi katika maovu, na neno lao litaenea kama donda-ndugu. Miongoni mwa hao wamo Himenayo na Fileto, walioikosa ile kweli, wakisema ya kwamba kiyama imekwisha kuwapo, hata kuipindua imani ya watu kadha wa kadha.”



Utangulizi:

Ni muhimu kufahamu kuwa tunaishi katika nyakati za mwisho sana, katika nyakati hizi, kumekuwepo na madhehebu mengi sana na kila dhehebu lina misimamo yake na mafundisho yake, hata hivyo kila Mkristo ana wajibu wa kuhakikisha kuwa yeye mwenyewe anakuwa na ujuzi wa kutosha kuhusu Neno la Mungu na namna linavyotumiwa ili aweze kupambanua nani analitumia neno la Mungu kwa halali na nani analitia maji, yaani kulighoshi, kughoshi ni Kiswahili cha zamani chenye maana ya kuongeza maji, mfano unapokuwa na maziwa halisi, sasa ili yawe mengi unaongeza na maji yaani kuchakachua, kwa hiyo katika nyakati zetu hizi vilevile tunao watu wanaolichakachua neno la Mungu hivyo kila mmoja anapaswa kuwa na akili ya kujua nani anachakachua neno na ni nani analitendea haki, huu ni wajibu wa kila Mkristo na kila mwanafunzi wa Yesu!

2Wakorintho 2:17 “Kwa maana sisi si kama walio wengi, walighoshio neno la Mungu; bali kama kwa weupe wa moyo, kama kutoka kwa Mungu, mbele za Mungu, twanena katika Kristo.”

Tatizo liliopo ni kuwa kila mtu duniani anaweza kuwa na tafasiri yake kuhusu neno la Mungu na akafikiri kuwa yuko sahihi, kwa sababu kila mtu anasema anaifuata Biblia anaiamini Biblia lakini wakati huo huo tunashuhudia kuwepo kwa tafasiri na misimamo tofauti tofauti kuhusu neno la Mungu, sasa basi, ikiwepo miongozo muhimu itatusaidia katika kulitumia neno la Mungu kwa halali na kuepuka changamoto nyingi zinazoweza kujitokeza, Mungu ni Mungu wa Utaratibu na sio Mungu wa Machafuko! Kwa hiyo ni wajibu wa Kila Mkristo kuyachunguza maandiko ili kujithibitishia kama kilichohubiriwa ni cha kweli bila kujali anayehubiri ni mtu wa namna gani au ana heshima kiasi gani hivyo ndivyo walivyokuwa watu waungwana katika kanisa la Baroya alipohubiri Paulo Mtume ona

Matendo 17:10-11 “Mara hao ndugu wakawapeleka Paulo na Sila usiku hata Beroya. Nao walipofika huko wakaingia katika sinagogi la Wayahudi. Watu hawa walikuwa waungwana kuliko wale wa Thesalonike, kwa kuwa walilipokea lile neno kwa uelekevu wa moyo, wakayachunguza maandiko kila siku, waone kwamba mambo hayo ndivyo yalivyo.”

Watu wa Beroya walikuwa waungwana, kwa mujibu wa Luka kwanini kwa sababu bila kujali nani anahubiri walifanya kazi ya kuyachunguza maandiko kila siku ili wajithibitishie kuwa yanayohubiriwa ni kweli? Mungu hapendezwi na makundi makubwa ya watu ambao wanabaki kuwa maamuma kila siku, wajinga wasio na mafunzo, wasiothibitishwa, wasio na ujuzi kwa kiingereza wanaitwa LAY waliolala au LAY PERSON  a person who is not trained, not qualified or not having an experience in a particular subject or activity  unaona kwa wakatoliki wanaitwa WALEI, Mungu hajatuita ili tuendelee kutengeneza kundi kubwa la watu wajinga Agizo kuu linatutaka kuwafanya watu wote kuwa wanafunzi, wawe wenye kufaa Qualified  wajue neno, wachambue neno, watafasiri neno wahoji maswali, wajibu maswali watengeneze mijadala yenye faida wawe wakomavu ! Waelimike

2Timotheo 4:1-4 “Nakuagiza mbele za Mungu, na mbele za Kristo Yesu, atakayewahukumu walio hai na waliokufa; kwa kufunuliwa kwake na kwa ufalme wake; lihubiri neno, uwe tayari, wakati ukufaao na wakati usiokufaa, karipia, kemea, na kuonya kwa uvumilivu wote na mafundisho. Maana utakuja wakati watakapoyakataa mafundisho yenye uzima; ila kwa kuzifuata nia zao wenyewe watajipatia waalimu makundi makundi, kwa kuwa wana masikio ya utafiti; nao watajiepusha wasisikie yaliyo kweli, na kuzigeukia hadithi za uongo

Waefeso 4:11-14 “Naye alitoa wengine kuwa mitume, na wengine kuwa manabii; na wengine kuwa wainjilisti na wengine kuwa wachungaji na waalimu; kwa kusudi la kuwakamilisha watakatifu, hata kazi ya huduma itendeke, hata mwili wa Kristo ujengwe; hata na sisi sote tutakapoufikia umoja wa imani na kumfahamu sana Mwana wa Mungu, hata kuwa mtu mkamilifu, hata kufika kwenye cheo cha kimo cha utimilifu wa Kristo; ili tusiwe tena watoto wachanga, tukitupwa huku na huku, na kuchukuliwa na kila upepo wa elimu, kwa hila ya watu, kwa ujanja, tukizifuata njia za udanganyifu.”

Kwa msingi huo leo tutachukua muda kutafakari na kujifunza kwa makini somo hili la thamani Kutumia kwa halali neno la kweli kwa kuzingatia vipengele vitatu vifuatavyo:-

·         Maana ya kutumia neno la Kweli kwa halali

·         Jinsi ya kutumia neno la kweli kwa halali

·         Kanuni za kutumia neno la kweli kwa halali

Maana ya kutumia neno la kweli kwa halali.

2Timotheo 2:15 “Jitahidi kujionyesha kuwa umekubaliwa na Mungu, mtenda kazi asiye na sababu ya kutahayari, ukitumia kwa halali neno la kweli.”

Paulo mtume alikuwa anamuagiza Timotheo aliyekuwa Askofu wa Makanisa ya Efeso kuhakikisha kuwa analitumie neno la Mungu yaani neno la Kweli kwa halali, Neno la kweli linalotajwa hapo ni Neno la Mungu yaani Biblia, kwa hiyo Mwalimu wa neno la Mungu anaagizwa hapo kuhakikisha kuwa analitumia kwa halali, nini maana ya kutumia neno la kweli kwa halali?

Ili tuweze kuelewa Mstari huu vizuri na kuweza kuweka msingi wa somo letu vizuri kwanza nitauweka mstari huu katika kiingereza

Study to shew thyself approved unto God, a workman that needeth not to be ashamed, rightly dividing the word of truth  

Kwa hiyo katika Biblia ya kingereza KJV ambayo ndiyo iliyotumika kuleta Biblia ya Kiswahili kwetu Mstari huo unasomeka namna hiyo, sasa nikianza na neno kutumia kwa halali neno la kweli, RIGHT DIVIDING tafasiri ya kiyunani ya neno hilo ni “ORTHOTOMOUNTA  ambalo ni neno la Kiyunani linaloundwa na misamiati miwili yaani “ORTHOS” na “TOMO” Orthos maana yake ni Perfectly right au Staright na neno Tomo ni CUT  kwa hiyo neno ORTHOTOMOUNTA maana yake mega sawa sawa, au kata sawasawa, au kata kwa ukamilifu,  maana yake hasa inatokana na asili ya kiroho ya neno kugawa mkate, au kuumega mkate

Matendo 2:46-47 “Na siku zote kwa moyo mmoja walidumu ndani ya hekalu, WAKIMEGA MKATE nyumba kwa nyumba, na kushiriki chakula chao kwa furaha na kwa moyo mweupe, wakimsifu Mungu, na kuwapendeza watu wote. Bwana akalizidisha kanisa kila siku kwa wale waliokuwa wakiokolewa.”

Neno la Mungu ndio Mkate wetu wenyewe kwa hiyo wakati wa kuuvunja mkate mvunjaji anatakiwa aukate sawasawa, kama vile watu wanavyokata keki na kutoa vipande vyenye uwiano ili kile kitakachomfikia mtu kiwe sawasawa bila upendeleo, kwa hiyo Lugha hii ndiyo inayotumiwa katika kuelezea namna tunavyopaswa kulitumia neno la Mungu kwa halali na sio kama kila mtu atakavyo au kila kanisa litakavyo au kila dhehebu litakavyo bali kama Mungu atakavyo ona

2Patro 1:19-20 “Nasi tuna lile neno la unabii lililo imara zaidi, ambalo, mkiliangalia, Kama taa ing'aayo mahali penye giza, mwafanya vyema, mpaka kutakapopambazuka, na nyota ya asubuhi kuzuka mioyoni mwenu. Mkijua neno hili kwanza, ya kwamba hakuna unabii katika maandiko upatao kufasiriwa kama apendavyo mtu fulani tu.”

Unaona? Kwa msingi huo sio sawa kwa mujibu wa maandiko kwamba kila mmoja ajitafasirie maandiko kama apendavyo hapana, haiko hivyo, huwezi tu kwenda kwenye maandiko na ukachukua tu chpchote unachoweza kuchukua na kuunga mkono mawao yako au njia yako, Mungu katika hekima yake ameweka namna ya kuyatafasiri maandiko na ndio maana kuna umuhimu wa kujifunza neno la Mungu kama tunavyoweza kuona katika kipengele kifuatacho, hilo sasa linatuleta katika kutafakari kipengele cha pili

Jinsi ya kutumia neno la kweli kwa halali

Mungu ni Mungu wa utaratibu na wala sio Mungu wa machafuko!, Mungu ndiye mwanzilishi wa Muda, aliuumba ulimwengu kwa siku sita, na kila siku ilikuwa ni masaa 24, Mungu aliumba ulimwengu na akaweka anga, leo hii kutokana na maendeleo makubwa ya kisayansi, tumegundua kuwa ziko sayari kadhaa ambazo hulizunguka jua, nazo zimewekewa utaratibu na ndio maana hazigongani! 1Wakorintho 14:40 “Lakini mambo yote na yatendeke kwa uzuri na kwa utaratibu.”

Taratibu zote zilizoko Duniani zimewekwa na Mungu, na wakati mwingine Mungu pia huweka watu wazazilishe au wasimamie utaratibu, ili mambo yote yatendeke kwa utaratibu, fikiria kwa mfano waliochinga baba bara kwa nchi zilizotawaliwa na uingereza magari barabarani hupita upande wa kushoto kwa njia ya kule linakoelekea gari, na zile zinazorudi hupita kushoto kwao ambako huwa ni kulia kwa anayekwenda, utaratibu wa namna hii pamoja na sharia zake barabarani ndio unaopelekea kuwepo kwa usalama na kupungua kwa matukio ya ajali,  jaribu kuwaza kama kusingelikuwa na utaratibu? Fikiria Hospitalini kwenye matibabu, Kama madaktari wangekuwa wanaandikia watu dawa hovyo hovyo, bila kuzingatia miaka, uzito, aina ya ugonjwa na dozi, je usalama wa wagonjwa ungekuwaje?  Mashuleni Kama kusingelikuwa na maswala ya hatua, wala silabasi wala walimu wa somo husika wala utaratibu wa vipindi kungekuwaje? Kungekuwa na machafuko na ukiangalia kwa makini utaweza kuona ilimutaratibu uweze kwenda vizuri watu wote hata madereva huwa wanaambiwa wasome, wasomee fani zao ili waweze kuufuata utaratibu uliokusudiwa katika Nyanja zao unaona?  Sasa ili neno la Mungu liweze kutumiwa kwa halali Paulo anamwambie Timotheo

2Timotheo 2:15 “Jitahidi kujionyesha kuwa umekubaliwa na Mungu, mtenda kazi asiye na sababu ya kutahayari, ukitumia kwa halali neno la kweli.”

Naomba tena niweke mstari huu katika kiingereza cha Biblia ya KJV King James Version mstari huo unasomeka hivi?

Study to shew thyself approved unto God, a workman that needeth not to be ashamed, rightly dividing the word of truth

Paulo mtume anapomwagiza Timotheo kutumia neno la Mungu kwa halali anaanza nan neno la Msingi kwenye Kiswahili JITAHIDI neno hilo KJV imetumia neno STUDY katika kiyunani ni SPOUDAZO ambalo maana yake ni BE DILIGENCE  yaani makinika, au chukua tahadhari zote au jielimishe study  kwa hiyo Mtafasiri wa maandiko au Mwalimu wa neno la Mungu anapaswa kutia bidi, kuwa makini, kusomea, kutafuta kwa bidi kutafasiri neno la Mungu kwa halali ili ampendeze Mungu, kama hatutakuwa makini na kila mtu akatafasiri maandiko anavyojisikia na atakavyo uelewa kuhusu Mungu na maagizo yake utakuwa haufanani duniani na neno hilo hilo litakuwa halijatumiwa kwa halali jambo litakalotuletea hukumu kubwa zaidi

Yakobo 3:1-2 “Ndugu zangu, msiwe waalimu wengi, mkijua ya kuwa mtapata hukumu kubwa zaidi. Maana twajikwaa sisi sote pia katika mambo mengi. Mtu asiyejikwaa katika kunena, huyo ni mtu mkamilifu, awezaye kuuzuia na mwili wake wote kama kwa lijamu.”             

Msiwe waalimu wengi kwa kiyunani DIDASKALOS  yaani  Doctors, Master teacher,  neno hilo limetumika kumtaja Yesu mara 40 kama Mwalimu Master na limejitokeza katika biblia mara 58 katima mistari tofauti 57 yote ikionyesha mtu aliyebobea katika kufundisha, Mtaalamu wa kutafasiri maandiko au Mwalimu wa neno anatakiwa awe mtu aliyebobea na ili mtu awe mbobevu anapaswa kuwa na bidi katika kujifunza na kujisomea, kwa hiyo kimsingi maandiko yanatutaka tuwe wabobezi yaani tusomee, na ndio maana katika vyoa vya Biblia liko somo maalumu kwaajili ya kusomea jinsi na namna nzuri ya kutafasiri neno la Mungu somo hilo linaitwa HERMENEUTICS, somo hilo haliwezi kufundishwa katika somo moja kama hivi, lakini hapa nakupa tu tahadhari ya kawaida ili ujue kuwa sio kila mtu anaweza kuwa Mwalimu wa neno la Mungu na kazi hii ni taaluma kama zilivyo taaluma nyingine, Upako jni wa Muhimu, lakini na upako unaweza kumilikiwa na mtu yeyote, karama ni za Muhimu nazo zinaweza kumilikiwa na mtu yeyote tu, hata hivyo, kutafasiri maandiko kunahitaji maarifa na ndio maana kuna walimu, kumbuka Naye alitoa wengine kuwa Mitume, manabii, wainjilisti, wachungaji na WALIMU kwa hiyo ni kazi ya wabobezi kutuingiza katika huo utaalamu wa kutafasiri maandiko HERMENEUTICS sio mtu anaamka tu na ndoto zake na anakuwa muhubiri, kama jinsi ambavyo Dakrati haamki tu na kuwa daktari ili ashughulikie miili ya watu hali kadhalika hainuki tu Mtu na kusema ni muhubiri na mtafasiri wa neno la Mungu kama kujifunza na kukaa chini ya walimu utakupuuzia tutakuwa na wazushi wengi sana katika karne hii, waalimu wote wazuri akiwepo Yesu mwenyewe walikaa chini nya walimu kwanza kabla ya kuwanza kuwa walimu wa neno la Mungu, wako watu ambao hujidhani kuwa ni wa kiroho sana na wanapuuzia sana swala la kusoma wakifikiri kuwa ni kupoteza Muda wako wanaodhani kuwa kwa kuwa wamejaa Roho Mtakatifu basi hawahitaji kujifunza hapana Roho wa Mungu huwa anaongoza watu wakajifunze kwanza kabla ya kuwatumia

-          Musa alipata Elimu ya kawaida kule Misri kwa umri wake wote miaka 40, na kisha alijifunza maswala ya kiroho kwa Kuhani wa Midian Yethro kwa miaka 40 jambo hili lilipelekea Musa kuwa Mwalimu mzuri sana na kiongozi aliyeandaliwa kuweka misingi ya kiroho, kisiasa, kisheria na maongozi na taratibu zote duniani Matendo 7:22 “Musa akafundishwa hekima yote ya Wamisri, akawa hodari wa maneno na matendo.”

 

-          Yesu Kristo Bwana wetu alikaa chini ya waalimu kabla ya kuwa Mwalimu ona Luka 2: 46-47 “Ikawa baada ya siku tatu wakamwona hekaluni, ameketi katikati ya waalimu, akiwasikiliza na kuwauliza maswali. Nao wote waliomsikia walistaajabia fahamu zake na majibu yake.” Unaona na zaidi ya yote alijifunza kwa Mungu Roho Mtakatifu nay eye alikaa na wanafunzi wake miaka mitatu na nusu ndipo akawaamuru wakahubiri injili

 

-          Paulo Mtume alikaa chini ya Mwalimu maarufu aitwaye Gamaliel Matendo 22:3 “Mimi ni mtu wa Kiyahudi, nalizaliwa Tarso, mji wa Kilikia, ila nililelewa katika mji huu, miguuni pa Gamalieli, nikafundishwa sheria ya baba zetu kwa usahihi, nikawa mtu wa jitihadi kwa Mungu kama ninyi nyote mlivyo leo hivi;” Paulo mtume licha ya kukaa chini ya Mwalimumaarufu Gamaliel na kujifunza maswala ya torati pia alikaa chini ya Roho Mtakatifu miaka 14 akijifunza injili aliyotukabidhi, ambayo alifundishwa na Yesu mwenyewe ona

 

Wagalatia 1:11-20 “Kwa maana, ndugu zangu, injili hiyo niliyowahubiri, nawajulisha ya kuwa siyo ya namna ya kibinadamu. Kwa kuwa sikuipokea kwa mwanadamu wala sikufundishwa na mwanadamu, bali kwa ufunuo wa Yesu Kristo. Maana mmesikia habari za mwenendo wangu zamani katika dini ya Kiyahudi, kwamba naliliudhi kanisa la Mungu kupita kiasi, nikaliharibu. Nami naliendelea katika dini ya Kiyahudi kuliko wengi walio hirimu zangu katika kabila yangu, nikajitahidi sana katika kuyashika mapokeo ya baba zangu. Lakini Mungu, aliyenitenga tangu tumboni mwa mama yangu, akaniita kwa neema yake, alipoona vema kumdhihirisha Mwanawe ndani yangu, ili niwahubiri Mataifa habari zake; mara sikufanya shauri na watu wenye mwili na damu; wala sikupanda kwenda Yerusalemu kwa hao waliokuwa mitume kabla yangu; bali nalikwenda zangu Arabuni, kisha nikarudi tena Dameski. Kisha, baada ya miaka mitatu, nalipanda kwenda Yerusalemu ili nionane na Kefa, nikakaa kwake siku kumi na tano. Lakini sikumwona mtume mwingine, ila Yakobo, ndugu yake Bwana. Na hayo ninayowaandikia, angalieni, mbele za Mungu, sisemi uongo.”      

 

Aidha licha ya kuwa alifundishwa na Yesu mwenyewe mtume huyu ambaye alikuwa mwana sharia pia alikuwa na bidi ya kujisomea na alisisitiza kuwa wahubiri wajisomee ona 2Timothy 4:13 “Lile joho nililoliacha kwa Karpo huko Troa, ujapo ulilete, na vile vitabu, hasa vile vya ngozi.”

 

Kwa hiyo Paulo anapomtaka Timotheo awe na bidii katika kujisomea alimaanisha kuwa huwezi kumtenga Muhubiri na tabia ya kujisomea, kutafakari na kuandaa neno la Mungu sawa na kanuni alizozikusudia Mungu, kila Muhubiri ni Mwalimu na hivyo kila Muhubiri anapaswa kusoma na kujisomea, kwenda shule na kuendelea kuwa na tabia ya kujisomea siku zote za maisha Yetu, kufundisha na kuwaelezea watu neno la Mungu hakupaswi kuwa kwa kukurupuka tu, Kanisani hakuna wajinga kuna watu wengine ni wasomi, wengine ni viongozi wengine wana akili wengine wana ujuzi, kwa hiyo sio mahali ambako utaokota biblia na kuondoa vumbi na kwenda kusema tu ili mradi unajua kusagia watu hapana kuna kanuni zake kuna hatua zake kuna utaratibu wake

 

Isaya 28:9-13 “Atamfundisha nani maarifa? Atamfahamisha nani habari hii? Je! Ni wale walioachishwa maziwa, walioondolewa matitini? Kwa maana ni amri juu ya amri, amri juu ya amri; kanuni juu ya kanuni, kanuni juu ya kanuni; huku kidogo na huku kidogo. La, bali kwa midomo ya watu wageni, na kwa lugha nyingine atasema na watu hawa; ambao aliwaambia, Hii ndiyo raha yenu, mpeni raha yeye aliyechoka; huku ndiko kuburudika; lakini hawakutaka kusikia. Kwa sababu hiyo neno la Bwana kwao litakuwa hivi, amri juu ya amri, amri juu ya amri; kanuni juu ya kanuni, kanuni juu ya kanuni; huku kidogo na huku kidogo; ili waende na kuanguka nyuma, na kuvunjwa, na kunaswa, na kuchukuliwa.”

 

Kwa hiyo watu wanaohudumia roho za watu hawapaswi kuwa watu wa kuokota okota tu hapana wanapaswa kuwa watu wenye akili timamu, sio waliochoka, wala vichaa bali watu wenye akili na wanaojua kujifunza walio hodari katika maandiko ili waweze kuijenga jamii kwa hiyo tusifikiri kuwa Mungu anafurahia neno lake lipotoshwe tu hata wewe unaweza kuwa mkali pale watu wanapokunukuu vibaya,Kama tunamuheshimu Mungu hatuna budi basi kuyaheshimu na mambo yake badala ya kuibuka tu kama uyoga na ukachezea roho za watu, tukifanya hivyo kutakuwa na uwiano sawia  wa ujuzi wa neno la Mungu kwani ndio maana Yesu aliagiza kuwafanya watu wote kuwa wanafunzi. Hilo sasa linatuleta katika mkutafakari kipengele cha tatu na cha mwisho

Kanuni za kutumia neno la kweli kwa halali

Kutafasiri neno la Mungu ni taaluma, ni sayansi, ni elimu na iko miiko ya jinsi na namna ya kulitafasiri neno la Mungu, kanuni hizo zikizzingatiwa kutakuwa na upungufu mkubwa wa tafasiri za neno la Mungu na watu hawatatafasiri maandiko kama wapendavyo tu bali sawa na kanuni zilizoainishwa na kupendekezwa kitaalamu, Sayansi hii ya kutafasriri neno la Mungu inaitwa Hermeneutics hermeneutics ni nini kwa kiingereza

1.       Hermeneutics is a branch of Science that deals with the interpretation of scriputres especially the Bible

2.       Hermeneutics ni tawi la Maarifa linalohusika na utaalamu (kanuni) wa kutafasiri maandiko hususani Biblia

Sina mpango wa kufundisha somo hilo hapa, kwani haya ni maubiri tu, lakini nataka kutoa maswala ya kuzingatia wakati mtu anataka kufundisha neno la Mungu au kuhubiri, hii ni kwaajili ya watu wa kawaida watu wote, sio kwaajili ya wahubiri na wachungaji waliokwenda au waliopo vyuoni japo nimezingatia sana kuwafaa watu wote kama Neno la Mungu lilivyo:-

Ni muhimu kufahamu kuwa kwa nini Biblia inahitaji tafasiri? Au kutumiwa kwa halali, tunaweza kusema kuwa je Mungu si amewakusudia watu wote wafikiwe na neno lake jibu ni ndio lakini watu hao wana Historia tofauti, tamaduni tofauti, lugha tofauti, na muda au nyakati tofauti kwa hiyo kuna vitu vya kuzingatia wakati mtu anataka kutafasiri neno la Mungu, ndio maana umeweza kuona kwa mfano Paulo anamwambia Timotheo JITAHIDI katika Kiswahili lakini katika kiingereza STUDY bila kucheza na lugha iliyokusudiwa unaweza kujikuta hupati maana iliyokusudiwa! Kwa hiyo Lugha, Tamaduni, Historia, na muda unaweza kuwa kwazo kwa Muhubiri na mtafasiri wa maandiko na ndio maana tunahitaji miongozo! Miongozo hiyo inatusaidia

1-      Kulijua wazo kamili la Mungu alilolikusudia katika neno lake

2-      Kuzuia tafasiri zisizo za kweli ya neno la Mungu

3-      Kuzuia kupotoshwa kwa lengo la injili

4-      Kuzuia hukumu ya Mungu

5-      Kuleta uwiano wa ufahamu na mwenendo na tabia kwa wanafunzi wa Yesu duniani

6-      Maandiko yanahitaji Mtafasiri au mfafanuzi juhudi ya kusoma pekee haitoshi mpaka mtu akufafanulie ona Matendo 8:30-31 Biblia inasema hivi “Ndipo Filipo akakimbilia na kumsikia yule mtu anasoma kitabu cha nabii Isaya. Filipo akamwuliza, Je, yanakuelea hayo usemayo? Yule towashi akasema, Nitawezaje kuelewa mtu asiponifafanulia? Hivyo akamkaribisha Filipo ili apande na kuketi pamoja naye”.

Kwa hiyo kumbe kanuni zitasaidia kwa kiwango kikubwa kupunguza au kuondoa kabisa changamoto na kutokuruhusu uzushi kulivamia kanisa la Mungu na kuondoa utata wa kiufahamu, kwa sababu Mungu anataka tuwe na nia moja

1.       Mtafasiri wa maandiko wakati wote anapaswa kuwa na NIA NJEMA Hakikisha kuwa una moyo safi, unakwenda katika maandiko kwa kusudi la kutafuta jambo jema la kuijenga jamii Matendo 24:16 “Nami ninajizoeza katika neno hili niwe na dhamiri isiyo na hatia mbele za Mungu na mbele ya watu siku zote.” Unaweza kuwa msomi na unaweza usiwe msomi, lakini Mungu huchunguza nia ya moyo, huiangalia dhamira, unapodhamiria kuifundisha kweli unajiweka salama mbele za Mungu na unapodhamiria kupotosha kama balaam Mungu anaiona nia yako, kwa hiyo ili mtu awe na nia njema na dhamiri safi ni lazima awe na hofu ya Mungu nah ii ikiwepo utalichukulia neno la Mungu kwa tahadhari kubwa.

 

2.       Neno la Mungu limevuviwa kwa sababu hiyo kila mtu mwenye nia njema na dhamiri safi anapotaka kulitumia kwa kusudi la kuwasaidia watu wa Mungu, kuwaonya, kuwakemea, na kuwakamilisha anaweza bado kuwa kwenye upande sahihi ona 2Timotheo 3:16-17 “Kila andiko, lenye pumzi ya Mungu, lafaa kwa mafundisho, na kwa kuwaonya watu makosa yao, na kwa kuwaongoza, na kwa kuwaadibisha katika haki; ili mtu wa Mungu awe kamili, amekamilishwa apate kutenda kila tendo jema.”

 

3.       Kumbuka kwamba maandiko yana tabia ya kujitafasiri yenyewe kwa msingi huo uko umuhimu wa kuzingatia andiko lingine na lingine linalolingana au kuunga mkono wazo la kile unachotaka kukisimamia, maana yake huwezi kuwa na fundisho linalotokana na Mstari mmoja kwa hiyo kila neno lithibitike kwa kina cha ushahidi wa maandiko mengine zaidi 2Wakorintho 13:1 “Hii ndiyo mara ya tatu ya mimi kuja kwenu. Kwa vinywa vya mashahidi wawili au watatu kila neno litathibitishwa.” Kwa hiyo mtafasiri wa maandiko anapaswa kuzingatia uwiano wa fundisho lake na maandiko mengine au na biblia nzima uwiano huo wa kimaandiko unaitwa  “cross references” yaani nukuu ya andiko moja ama linguine linalofanana na lile unalotaka kuelezea fundisho lako

 

4.       Wakati mwingine ni salama Kurahisisha maandiko kwa kuyachukua kama yalivyo badala ya kufikiri kuwa kila andiko ni fumbo, watu wengi wanaodhani kuwa maandiko ni mafumbo wanaweza kushawishika kutafasiri kila kitu hata vile ambavyo havihitaji tafasiri, na matokeo yake wanapotosha, Hata hivyo ni muhimu kuchukua tahadhari kwani pia sio kila andiko unaweza kulichukua kama lilivyo kwa mfano

 

2Wafalme 6:25 “Biblia ya Kiswahili inasema hivi Njaa ikawa kuu huko Samaria; na tazama, wakauhusuru, hata kichwa cha punda kikapata kuuzwa kwa vipande themanini vya fedha, na kibaba cha mavi ya njiwa kwa vipande vitano vya fedha.”

 

Unapoona neno Kibaba cha mavi ya njiwa na ukachukua neno hilo kama lilivyo ni rahisi kufikiri kuwa Samaria kulikuwa na njaa mpaka mavi ya njiwa yaliuzwa! Jambo hilo sio sahihi na hapo ndipo unapoweza kuona umuhimu wa sayansi ya kutafasiri maandiko, andiko hilo hilo ukilisoma katika biblia ya kiingereza linasomeka hivi

 

2Kings 6:25 “There was agreat famine in the city; the siege lasted so long that a donkey’s head sold for eighty shekels of silver and quarter of a cab of seed pods for five shekels

 

Unapoanza tu kuangalia andiko hilo kitaalamu kwa kuanza kuangalia Lugha iliyotumika katika matoleo tofauti tofauti ya buiblia utagundua kuwa neno KIBABA CHA MAVI YA NJIWA, kwa kiingereza CUB OF SEED maana yake ni KIBAKULI CHA MBEGU kwa hiyo kwa maamuma kuchukua njia rahisi au kurahisisha tu kunaweza kuwa salama na kunaweza kuwa hatari ndio maana maandiko yanahitaji wataalamu.

 

5.       Andiko au mstari unaotaka kuubiri au kuutumia lazima uzingatie wazo zima MUKTADHA wa kile kilichokuwa kinazungumziwa hapo karibu na wazo zima la kibiblia, huwezi kuchukua nyuzi moja na kuiita nguo, nguo ni mkusanyiko wa nyuzi nyingi. Hakuna andiko lolote katika Biblia ambalo likitafasiriwa vizuri kwa kuzingatia Mazingira yake MUKTADHA litaleta utata wa kimaandiko. Na kama utata utatokea basi mtafasiri atapaswa kuelezea utata huo, bila kutafuta kupuuzia ukweli unaofunuliwa na andiko hilo

6.       Panua ufahamu wako kuhusu Lugha na matumizi ya lugha katika Biblia kuna lugha za mafumbo Kuna aina mbalimbali za Lugha za mafumbo zinzotumika katika Biblia inasemekana ziko lugha za mafumbo zilizotumika katika Biblia zaidi ya 200 pamoja na mifano yake ipatayo 800 lugha hizo za mafumbo ni kama vile:-

·         Misamiati – (Vocabulary)

·         Mifano na fumbo la maneno  (Parable and allegories)

·         Ulinganisho unaotumia maneno  kama,  na na ulinganishi usiotumia neno kama na (Similes and Metaphors)

·         Maneno ya kuongoza chumvi (Hyperboles)

·         Maneno ya kuhuisha au kukipa kitu au mnyama uhai au ubinadamu ( Personification)

·         Kumliganisha Mungu na mwanadamu (Antropomorphism)

·         Jina moja kwa niaba ya linguine (Metonymy)

·         Sehemu moja kwa jambo lote au Sehemu nzima kwa sehemu (synecdoche)

·         Kuzungumza kinyume cha uhalisia ( Irony)

·         Lugha za mficho  inayotumika badala ya neno chafu Figurative language au (Euphemism )

·         Mithali (Proverbs)

 

7.       Uwe na ufahamu wa kutosha kuhusu uhusiano ulioko kati ya agano la kale na agano jipya na ni matumizi yapi ya kiagano yanatumika mpaka sasa na yasiyotumika mpaka sasa na yaliyosalia vile vile

8.       Uwe na ufahamu wa kihistoria wa andiko na maana iliyokusudiwa na mwandishi na namna inavyoweza kutumika katika nyakati za leo

9.       Uwe na ufahamu wa jinsi na namna ya kutafasiri mifano ya kibiblia

10.   Uwe na ufahamu wa jinsi na namna ya kutafasiri unabii, kujua yaliyokwisha kutimizwa na ambayo badio hayajatimizwa

Hitimisho.

Hiyo ni miongozo tu ambayo inamsaidia mtu anayetaka kutafasiri maandiko kuweza kuizingatia ili aweze kulileta neno la Mungu kwa usahihi, Mtafasiri wa maandiko pia anapaswa kuwa na Nyenzo mbalimbali zinazoweza kusaidia katika kazi hii ya kutafasiri maandiko Nyenzo hizo ni pamoja na

NYENZO MUHIMU ZINAZOSAIDIA KATIKA KUYATAFASIRI MAANDIKO KWA USAHIHI

ROHO MTAKATIFU:

Ni nyenzo ya kwanza na ya Muhimu sana mtu awaye yote anayetaka kuwa mtafasiri mzuri wa Maandiko ni lazima akubali kujazwa Roho Mtakatifu kumbuka kuwa yeye ndiye aliyevuvia watu kuliandika neno na ni mwalimu anaweza kutukumbusha na kutufundisha kile ambacho Mungu amekikusudia kwetu hivyo lazima mtafasiri wa maandiko awe amejazwa Roho ikiwa wale waliokuwa mashemasi nyakati za kanisa la kwanza walizingatiwa kuwa wenye Roho je si zaidi sana wanaojitia katia kazi ya kuyatangaza Maandiko ona mfano wa Stefano Matendo 6;8-55 kwanini ni muhimu kuwa na Roho mtakatifu?

·         Ni Mtafasiri mzuri

·         Ndiye Mwandishi wa Biblia

·         Anajua kile Ambacho Mungu anakijua

HAKIKISHA KUWA UNA BIBLIA ZA MATOLEO TOFAUTI

·         Biblia ya Kiswahili na za aina mbalimbali za matoleo ya kiswahili cha kisasa             

·         English Bible matoleo tofauti

·         Zile zilizoandikwa katika Lugha Tofauti Tofauti (Greek, Hebrew, Latin, Aramaic, na kadhalika)

UWE NA UJUZI KUHUSU AINA ZA MATOLEO YA BIBLIA

Kwa kawaida kuna matoleo makuu ya aina tatu za kibiblia zile zilizotafasiri neno kwa neno Literal translations, Zile zilizotafasiri kutokana na maana iliyokusudiwa, Dynamic Equivalent na zile tafasiri huru za lugha za kisasa Free translation mfano

                     Literal translations.           Dynamic Equivalence translations.      Free translations

                       Neno kwa neno                             Maana kwa maana                          Tafasiri huru

UWE NA BIBLIA ZENYE MAFUNZO NDANI YAKE; STUDY BIBLES,  REFERENCE OR ANNOTATED

Uwe na Biblia zenye mafunzo Studies Bible Zinatoa maana ya baadhi ya aya:

1.                   Mfano mzuri ni Full life study Bible (NIV) Biblia ya mafunzo ya uzima tele

2.                   Life Application Bible (LB)

3.                   Dake Bible

4.                   Scafield Bible, na kadhalika  

Uwe na  uchambuzi wa kibiblia wa watu wa aina mbalimbali COMMENTARIES: (Zenye uchambuzi wa mstari kwa mstari au kifungu kwa kifungu na kadhalika ).

Baadhi ya Commentaries nzuri kwa mfano ni Pamoja na

1.       Adam Clarke’s Commentary

2.       The New International Commentary

3.       The Evangelical Bible Commentary

4.       Mathew Henry Commentary.

Uwe na kitabu chenye ulinganifu wa kila neno katika biblia kuanzia a mpaka z CONCORDANCES   ITIFAKI

    • Itifaki yenye maneno yafananayo
    • Itifaki za maana ya meneno mfano  Malazi yawe safi -Ndoa
    • Mlinganio wa maneno yanayopatikana katika sehemu nyingine za Biblia.
    • Mfano Upendo upi? – Agape? Phileo? Storge? Eros?
    • Mahali lilipo neno Fulani

Mfano wa itifaki nzuri ni pamoja na ;-

o   Young’s Analytical Concordance

o   Strong’s Exhaustive Concordance etc.

o   Niv Exhaustive Concodance.

o   Kumbuka nyingine zina Kamusi za  kiibrania na Kiyunani  Lexicons (=Dictionaries )

Uwe na VITABU VINAVYOHUSU TAMADUNI ZA KIBIBLIA & MASWALA YA UCHIMBAJI WA   MAMBO YA KALE

Hii itakusaidia kuufahamu na kuwa na ujuzi kuhusu mambo ya kale kama na maneno yaliyotumiwa kama Busu takatifu, Tundu la sindano na mambo mengineyo.

KAMUSI ZA BIBLIA NA ZA LUGHA ZA KAWAIDA & ENCYCLOPAEDIAS:

Zinafafanua maana ya maneno Mbalimbali kwa ajili ya maswala ya kibiblia na maswala ya kawaida

1.            Kamusi za kawaida ni pamoja na zile za Kiingereza na kiswahili

·         English Language Dictionary

·         Swahili Language Dictionary etc. (Kamusi)

2.            Kamusi za Biblia ni pamoja na zilizo maarufu kama zifuatazo nyingi ni za kiingereza

·         Unger’s Bible Dictionary                                       

·         Pictorial Bible Dictionary                                       

·         Westminster Bible Dictionary                                  

·         Greek Lexicon & Hebrew Lexicon                        

·         Kamusi za kitheolojia (Theological Dictionary).

·         Kwa ajili ya kujifunza Mambo mbalimbali ya kitheolojia Mfano ni

·          Baker’s Dictionary of Theology

4.            Encyclopedias,

                Mfano; - International Standard Bible Encyclopedia

Uwe na MAFAFANUZI YA KIBIBLIA (BIBLE HANDBOOKS :)

Kwa ajili ya ufafanuzi wa Maswala mbalimbali, Vifungu, Maandiko, Tamaduni, Matukio ya kihistoria,  Ugunduzi wa maswala ya kale (archaeology), na kadhalika

Mfano

·         Halley’s Bible Hand Book

·         Unger’s Bible Hand Book

Uwe na MASOMO MBALIMBALI AU JUMBE MBALIMBALI (TOPICAL BIBLE).

Vitabu vinavyo weka mpangilio wa ufafanuzi wa masomo mbalimbali vikiwa na maandiko yoote husika sawa book arranged according to different topics with all the texts related to each topic.

Mfano Nave’s topical Bible

Uwe na ATLASI ZA KIBIBLIA NA MSWALA YA KIHISTORIA (BIBLE ATLASS) & HISTORY

Kwa ajili ya kutambua sehemu Mbalimbali na umbali kwa kilomita za mraba n.k na vipimo kama homeri, yadi, mwendo wa sabato, Ridhaa n.k

·         Baker’s Bible Atlas

·         The Oxford Bible Atlas

Uwe na tabia ya kusoma Biblia, kusikiliza mahubiri ya wahubiri wengine, kuwa na akili ya kusoma vitabu mbalimbali na kupoanua maarifa kila wakati na kila siku, penda kujifunza na kufundisha na hakikisha kila wakati unakua na jambo jipya la kushirikiana na wengine

Na Rev. Innocent  Samuel Kamote

Mkuu wa wajenzi mwenye Hekima

0718990796.



Maoni 2 :

Pastor Samwel S.M alisema ...

Nashukuru kwa somo hili hakika limekaa vema.
Ila kuna kitu nimekiona bado natamani kujua zaidi hasa pale kwenye 2 wafalme 6:25,kwa namna nilivyofuatilia tafsiri za kiingereza nimeon NIV PEKEE ndo iko tofauti na tafsri zingine za kiingereza. Mwalimu ni tafsri gani bora ya kiingereza ambayo inafaa sana kuwa refence kwetu sisi tunaojifunza ili kupata tafsiri halisi ya biblia yetu ya kiswahili. Naomba ufafanuzi Rev. Innocent.

Mkuu wa Wajenzi Mwenye Hekima alisema ...


Hongera sana Pastor Samweli SM kwa kufuatilia mafundisho haya, tafasiri ya kiingereza ya NIV inaangulia katika kundi la Dynamic Translation ambapo mtafasiri anasoma maana ya sentensi nzima kisha anaitafasiri katika lugha yake

wakati tafasiri ya kiingereza ya KJV inaangukia katika kundi la Literal Translation ambapo mtafasiri alitafasiri neno kwa neno

wote walikuwa wazuri na wote walikuwa na nia njema kwa wachungaji ni Muhimu kuwa na tafasiri mbalimbali kwani kuna wakati unaweza kukuta tafasiri fulani imekaa vizuri zaidi kulingna na mahitaji nyako au ya Roho Mtakatifu kile anataka ukisema kwa watu kwa hiyo utatoa nukuu kutoka katika tafasiri inayokubaliana na lengo lako au la Mungu kwa jamii yako kwa wakati huo