Jumanne, 9 Aprili 2024

Hata saa tisa!

Mathayo 27:45-50 “Basi tangu saa sita palikuwa na giza juu ya nchi yote hata saa tisa. Na kama saa tisa, Yesu akapaza sauti yake kwa nguvu akisema, Eloi, Eloi, lama sabakthani? Yaani, Mungu wangu, Mungu wangu, mbona umeniacha?  Na baadhi yao waliohudhuria, waliposikia, walisema, Huyu anamwita Eliya. Mara mmoja wao akaenda mbio, akatwaa sifongo, akaijaza siki, akaitia juu ya mwanzi, akamnywesha. Wale wengine wakasema, Acha; na tuone kama Eliya anakuja kumwokoa. Naye Yesu akiisha kupaza sauti tena kwa nguvu, akaitoa roho yake.”



Utangulizi:

Moja ya matukio muhimu tunayoweza kuyazingatia katika msimu wa kukumbuka Mateso ya Bwana wetu Yesu Kristo, Kifo chake na kufufuka kwake ni Pamoja na Saa ile aliyokata roho, yaani saa tisa, Karibu kila mwandishi wa Injili anaonyesha tukio hili la kipekee la Yesu kukata roho saa tisa, licha ya kuwepo kwa giza kubwa na la kipekee kuanzia saa sita mpaka saa tisa na kisha saa tisa Ndipo Yesu alikata roho. Tunaweza kuona, tukio hilo likirudiwa tena na tena katika injili nyingine:-

Marko 15:33-34 “Na ilipokuwa saa sita, palikuwa na giza juu ya nchi yote, hata saa tisa. Na saa tisa Yesu akapaza sauti yake kwa nguvu, Eloi, Eloi, lama sabakthani? Maana yake, Mungu wangu, Mungu wangu, mbona umeniacha?”

Luka 23:44-46. “Hapo ilikuwa yapata saa sita, kukawa giza juu ya nchi yote hata saa kenda, jua limepungua nuru yake; pazia la hekalu likapasuka katikati. Yesu akalia kwa sauti kuu, akasema, Ee Baba, mikononi mwako naiweka roho yangu

Tukio la Yesu Kristo kufa saa tisa jioni lina umuhimu mkubwa sana kwa mujibu wa injili na ndio maana limeelezwa na injili zote tatu, tunaelezwa kuwa katika muda huo tofauti na kawaida kulikuwa na giza tangu saa sita hata saa tisa, na saa tisa Yesu alipaza Sauti ya kilio Mungu wangu Mungu wangu Mbona umeniacha, na kisha Yesu alifikia hatua ya kutimiza kusudi lote la ukombozi wa mwanadamu kwa kujitoa dhabihu yeye mwenyewe, kwa ukombozi wa Mwanadamu. Lakini labda swali muhimu linaweza kubakia pale pale kwa nini saa tisa? hilo linatupa nafasi ya kutafakari somo hili hata saa tisa kwa kuzingatia vipengele muhimu vitatu yafuatayo:-


·         Saa tisa katika masimulizi ya kale ya tamaduni za kiyahudi

·         Saa tisa kwa mujibu wa maandiko

·         Hata saa tisa!

 

Saa tisa katika masimulizi ya kale ya tamaduni za kiyahudi

Kwa mujibu wa masimulizi ya Kale Wayahudi waliamini kuwa Mungu alikuwa na tabia ya kumtembelea Adamu katika Bustani ya Edeni, Saa ya jua kupunga, Kwa kiingereza “In the cool of the day” Ruach/yom

Mwanzo 3:8-9 “Kisha wakasikia sauti ya BWANA Mungu, akitembea bustanini wakati wa jua kupunga; Adamu na mkewe wakajificha kati ya miti ya bustani, BWANA Mungu asiwaone. BWANA Mungu akamwita Adamu, akamwambia, Uko wapi?  

Kwa mujibu wa masimulizi ya kiyahudi Muda au wakati wa jua kupunga katika unaitwa YOM ambalo kwa tafasiri wakati wa  jioni ambapo wayahudi walikuwa wanaamini ni mida ya saa tisa, Kwa mujibu wa masimulizi ya kiyahudi Muda huu kwa kawaida Mbingu huwa zinafunguka, na Mungu huwa ana kuwa na shauku ya kuimarisha uhusiano wake na wanadamu, hili ni moja ya jambo la kwanza na muhimu ambalo tunalipata katika Masimulizi ya kiyahudi na ndio maana moja ya saa za maombi katika jumuiya ya kiyahudi ni pamoja na kuomba saa tisa. Meno mawili ya kiebrania yanatumika kuelezea Saa ya jua kupunga in the cool of the day ambalo ni Ruach na Yom yakiwa na maana wakati wa utembeleo wa Roho wa Mungu.

Aidha kweli nyingine ya Masimulizi ya kale ya kiyahudi inasema ni katika muda huu, Mungu alimpa Adamu usingizi Mzito na kuchukua sehemu ya ubavu wake na kumuumba Mwanamke.

Mwanzo 2:21-23 “BWANA Mungu akamletea Adamu usingizi mzito, naye akalala; kisha akatwaa ubavu wake mmoja, akafunika nyama mahali pake, na ule ubavu alioutwaa katika Adamu BWANA Mungu akaufanya mwanamke, akamleta kwa Adamu. Adamu akasema, Sasa huyu ni mfupa katika mifupa yangu, na nyama katika nyama yangu, basi ataitwa mwanamke, kwa maana ametwaliwa katika mwanamume.”

 Usingizi mzito katika lugha ya kiibrania wanatumia neno TARDEMA ambalo maana yake ni hali inayosababishwa na Mungu mwenyewe kwaajili ya kumletea mwanadamu ufunuo muhimu, au kufanya jambo la Muhimu kwa mwanadamu    
          

Masimulizi mengine ni kuwa saa tisa ni muda ambao wayahudi walikuwa wanautumia kwa maombi, kuna vipindi vikubwa vitatu vya maombi katika tamaduni za kiyahudi. Hata manabii na waandishi wa zaburi wana nukuu kadhaa katika maandiko, zinazoashiria kuwa wayahudi walikuwa na vipindi vitatu vya maombi na ambavyo wameendelea kuwa navyo hata siku za leo angalia

Zaburi 55:16-17 “Nami nitamwita Mungu, Na Bwana ataniokoa; Jioni, asubuhi, na adhuhuri nitalalama na kuugua, Naye ataisikia sauti yangu.”

Daniel 6:10-11 “Hata Danieli, alipojua ya kuwa yale maandiko yamekwisha kutiwa sahihi, akaingia nyumbani mwake, (na madirisha katika chumba chake yalikuwa yamefunguliwa kukabili Yerusalemu;) akapiga magoti mara tatu kila siku, akasali, akashukuru mbele za Mungu wake, kama alivyokuwa akifanya tokea hapo.Basi watu hao wakakusanyika pamoja, wakamwona Danieli akiomba dua, na kusihi mbele za Mungu wake   
  

Vipindi hivyo vitatu vya ibada za maombi, ambavyo Wayahudi wanaendelea navyo mpaka leo kwa lugha ya asili ya Kiibrania vinaitwa SHACHARIT, MINCHA NA MAARIV ambavyo tunavichambua kama ifuatavyo:-

1.       Shacharit: - huu ni muda wa maombi ya alfajiri ambapo Wayahudi husali baada ya kupambazuka kwa jua, Maombi haya hufikiriwa kuwa ni maombi ya muhimu sana ambayo wayahudi huamini kuwa wanapokea Baraka kubwa sana, maombi au sala ya alfajiri huambatana na Kusifu, kusoma maandiko hususani Torati. Na hii inasadikiwa kufanyika kati ya muda wa asubuhi mpaka saa tatu na hasa kilele chake ni saa tatu.

 

2.       Mincha: - huu ni Muda wa maombi ya jioni (afternoon) Maombi haya ndiyo ambayo hufanywa saa tisa, ni maombi mafupi sana, ukilinganisha na Maombi ya alfajiri yaani Sacharit, maombi haya ya saa tisa hujumuisha kuomba, kusoma zaburi na kunyamaza kimyaa (Amidah) kusimama kimyaa, nah ii inasadikiwa kufanyika kati ya saa sita mpaka saa tisa na kilele chake hasa kilikuwa saa tisa

 

3.       Maariv au Arvit: Maariv pia huitwa Maarib au Magharibi kwa Kiswahili, Maombi haya yanafanyika baada ya jua kuzama ni kwaajili ya kuukaribisha usiku na kuuaga mchana, maombi haya hujumuisha Baraka, na ukiri wa SHEMA ukiri wa shema ni ukiri unaopatikana katika Kumbukumbu la torati 6:4-5 nimenukuu hapa:-

 

Kumbukumbu 6:4-5 “Sikiza, Ee Israeli; Bwana, Mungu wetu, Bwana ndiye mmoja. Nawe mpende Bwana, Mungu wako, kwa moyo wako wote, na kwa roho yako yote, na kwa nguvu zako zote.”

 

Shema ndio kiini kikuu cha Imani ya kiyahudi, Maombi haya ya Maariv au magharibi kilele chake ni jioni saa kumi na mbili wakati wa kuzama kwa jua.

Kwa hiyo kwa mujibu wa tamaduni za kiyahudi, na dini ya kiyahudi, yanashikiliwa na wayahudi katika maisha yao yote na siku zote, Kwa hiyo kuna saa tatu, kuna saa tisa na kuna saa kumi na mbili, Kwa hiyo  Saa tisa ni moja ya saa nyeti katika tamaduni na dini ya kiyahudi. Wayahudi wengi waliamini kuwa muda huu ni muda mwema sana Saa tisa Muda wa dhabihu ya jioni Mungu husikia kwa haraka sana na hujibu kwa haraka sana, na ni saa ya miujiza mikubwa.

Zaburi 141:1-2 “Ee Bwana, nimekuita, unijie hima, Uisikie sauti yangu nikuitapo. Sala yangu ipae mbele zako kama uvumba, Kuinuliwa mikono yangu kama dhabihu ya jioni.”                        

Saa tisa kwa mujibu wa maandiko:

Nadhani sasa unaweza kupata picha ya umuhimu was aa tisa, ya kwamba ni saa yenye neema ya ajabu, ni saa yenye faida kubwa sana, kila mtu aliyeokolewa ana neema kubwa na amepewa neema ya kuzijua siri za ufalme wa Mungu, lakini kufunuliwa kwa nguvu za ufalme wa Mungu kunategemeana sana na ujuzi wa kanuni, kama vile ambavyo ziko hesabu huwezi kuzifanya bila kujua kanuni, au huwezi kupata majibu bila kujua kanuni, ufunuo kuhusu kanuni unatofautiana kati ya Mtu na mtu, Kadiri unavyozijua kanuni hizo ndio unajiweka katika nafasi kubwa sana ya mafanikio na siri za ufalme wa Mungu na kufaidika kiroho, kwa hiyo maombi ya saa tisa ni ufunuo wa Muhimu sana kwako leo, lakini ili uweze kuwa na ufahamu sasa tufuatane nani katika maandiko kuweza kuona saa hii kwa mujibu wa maandiko:-

-          Ulikuwa ni Muda ambao Bwana alimtembelea Ibrahimu na kuwa na ushirika naye pamoja na Sarah Na kumuahidi kupata mtoto Mwanzo 18:1-2 “BWANA akamtokea Ibrahimu karibu na mialoni ya Mamre, alipokuwa ameketi mlangoni pa hema yake mchana wakati wa hari. Akainua macho yake akaona, na tazama, watu watatu wamesimama mbele yake. Naye alipowaona alipiga mbio kuwalaki kutoka mlangoni pa hema, akainama mpaka nchi, akasema, BWANA wangu, kama nimeona fadhili machoni pako nakuomba usinipite sasa mimi mtumwa wako.” Neno Mchana wakati wa Hari katika kiibrania linatumika tena neno YOM ambalo lina maana ya jioni mida ya saa tisa

 

-          Ulikuwa ni Muda ambao makuhani waliagizwa kutoa dhabihu ya jioni Kutoka 29:38-42 “Basi sadaka utakazozitoa juu ya madhabahu ni hizi; wana-kondoo wa mwaka mmoja wawili siku baada ya siku daima. Mwana-kondoo mmoja utamchinja asubuhi; na mwana-kondoo wa pili utamchinja jioni; tena, pamoja na mwana-kondoo mmoja utatoa vibaba vitatu vya unga mzuri uliochanganyika na mafuta yenye kupondwa, kiasi cha kibaba na robo kibaba; na divai kiasi cha kibaba na robo kibaba, iwe sadaka ya kinywaji. Na huyo mwana-kondoo wa pili utamchinja wakati wa jioni, nawe utamfanyia vivyo kama ile sadaka ya unga ya asubuhi, na kama ile sadaka yake ya kinywaji, iwe harufu nzuri, ni dhabihu ya kusongezwa kwa BWANA kwa njia ya moto. Itakuwa ni sadaka ya kuteketezwa milele katika vizazi vyenu vyote mlangoni pa ile hema ya kukutania mbele ya BWANA; hapo nitakapokutana nanyi, ili ninene na wewe hapo.”

 

-          Ulikuwa ni Muda wa kuchoma au kufukiza uvumba wakati wa dhabihu ya jioni Kutoka 30:7-8 “Na Haruni atafukiza uvumba wa manukato juu yake; KILA SIKU ASUBUHI atakapozitengeneza zile taa, ataufukiza. Na Haruni atakapoziwasha zile taa WAKATI WA JIONI, ATAUFUKIZA, UWE UVUMBA WA DAIMA mbele za BWANA katika vizazi vyenu vyote.”

 

2Nyakati 13:11 “nao humtolea Bwana kila asubuhi, na kila jioni, sadaka za kuteketezwa na fukizo la manukato; mikate ya wonyesho pia huiweka kwa taratibu yake juu ya meza takatifu, na kinara cha dhahabu chenye taa zake, kuwaka kila jioni; kwa maana sisi twayalinda malinzi ya Bwana, Mungu wetu; bali ninyi mmemwacha.”

 

Luka 1:8-14 “Basi ikawa, alipokuwa akifanya kazi ya ukuhani katika taratibu ya zamu yake mbele za Mungu, kama ilivyokuwa desturi ya ukuhani, kura ilimwangukia kuingia katika hekalu la Bwana ili kufukiza uvumba. Na makutano yote ya watu walikuwa wakisali nje saa ya kufukiza uvumba. Akatokewa na malaika wa Bwana, amesimama upande wa kuume wa madhabahu ya kufukizia. Zakaria alipomwona alifadhaika, hofu ikamwingia. Lakini yule malaika akamwambia, Usiogope, Zakaria, maana dua yako imesikiwa, na mkeo Elisabeti atakuzalia mtoto mwanamume, na jina lake utamwita Yohana.Nawe utakuwa na furaha na shangwe, na watu wengi watakufurahia kuzaliwa kwake.”

 

-          Ulikuwa ni Muda ambao Eliya alimuomba Mungu dhidi ya manabii wa baali katika mlima Karmel na Mungu akamjibu kwa moto kutoka mbinguni 1Wafalme 18:36-39 “Ikawa, wakati wa kutoa dhabihu ya jioni, Eliya nabii akakaribia, akasema, Ee Bwana, Mungu wa Ibrahimu, na wa Isaka, na wa Israeli, na ijulikane leo ya kuwa wewe ndiwe Mungu katika Israeli, na ya kuwa mimi ni mtumishi wako, na ya kuwa nimefanya mambo haya yote kwa neno lako. Unisikie, Ee Bwana, unisikie, ili watu hawa wajue ya kuwa wewe, Bwana, ndiwe Mungu, na ya kuwa wewe umewageuza moyo wakurudie. Ndipo moto wa Bwana ukashuka, ukaiteketeza sadaka ya kuteketezwa, na kuni, na mawe, na mavumbi, ukayaramba yale maji yaliyokuwamo katika mfereji. Na watu wote walipoona, wakaanguka kifudifudi; wakasema, Bwana ndiye Mungu, Bwana ndiye Mungu.”

 

-          Ulikuwa ni Muda huu ambao Ezra aliomba Maombi ya toba na maombezi yaliyoleta uamsho mkubwa sana miongoni mwa jamii ya Wayahudi waliokuwa wamerudi nyuma Ezra 9:4-8 “Ndipo wakanikusanyikia watu wote walioyatetemekea maneno ya Mungu wa Israeli, kwa sababu ya lile kosa la watu wa uhamisho; nami nikaketi kwa mshangao hata wakati wa sadaka ya jioni. Na wakati wa sadaka ya jioni nikainuka baada ya kunyenyekea kwangu, nguo yangu na joho yangu zimeraruliwa, nikaanguka magotini nikakunjua mikono yangu mbele za Bwana, Mungu wangu; nikasema, Ee Mungu wangu, nimetahayari, naona haya kuinua uso wangu mbele zako, Mungu wangu; kwa maana maovu yetu ni mengi, hata yamefika juu ya vichwa vyetu, na hatia yetu imeongezeka na kufika mbinguni. Tangu siku za baba zetu tumekuwa na hatia kupita kiasi hata leo; na kwa sababu ya maovu yetu sisi, na wafalme wetu, na makuhani wetu, tumetiwa katika mikono ya wafalme wa nchi hizi, tumepigwa kwa upanga, tumechukuliwa mateka, tumenyang'anywa mali zetu, tumetiwa haya nyuso zetu, kama hivi leo. Na sasa kwa muda kidogo tumeneemeshwa na Bwana, Mungu wetu, hata akatuachia mabaki yaokoke, akatupa msumari katika mahali pake patakatifu. Mungu wetu atutie nuru machoni mwetu, tuburudike kidogo katika kufungwa kwetu.”

 

-          Ulikuwa ni Muda ambao Daniel nabii aliletewa majibu ya maombi yake kupitia malaika Gabriel Daniel 9:20-22 “Basi hapo nilipokuwa nikisema, na kuomba, na kuiungama dhambi yangu, na dhambi ya watu wangu Israeli, na kuomba dua yangu mbele za Bwana, Mungu wangu, kwa ajili ya mlima mtakatifu wa Mungu wangu; naam, nilipokuwa nikinena katika kuomba, mtu yule, Gabrieli, niliyemwona katika njozi hapo kwanza, akirushwa upesi, alinigusa panapo wakati wa dhabihu ya jioni. Akaniagiza, akaongea nami, akasema, Ee Danieli, nimetokea sasa, ili nikupe akili upate kufahamu.”

 

-          Ulikuwa ni Muda ambao Yesu Kristo alikuwa ameimaliza kazi yote Pazia la hekalu lilipasuka na Yesu akakata roho kwa kuikabidhi roho yake mikononi mwa Baba Luka 23:44-46. “Hapo ilikuwa yapata saa sita, kukawa giza juu ya nchi yote hata saa kenda, jua limepungua nuru yake; pazia la hekalu likapasuka katikati. Yesu akalia kwa sauti kuu, akasema, Ee Baba, mikononi mwako naiweka roho yangu

 

-          Ulikuwa ni Muda ambao Petro na Yohana walikuwa wakihudhuria maombi katika hekalu na Kiwete akaponywa na ukawa ndio muujiza wa kwanza katika kanisa la kwanza ulioambatana na uamsho mkubwa na kuokolewa kwa watu wengi zaidi Matendo 3:1-7 “Basi Petro na Yohana walikuwa wakikwea pamoja kwenda hekaluni, saa ya kusali, saa tisa. Na mtu mmoja aliyekuwa kiwete toka tumboni mwa mamaye alichukuliwa na watu, ambaye walimweka kila siku katika mlango wa hekalu uitwao Mzuri, ili aombe sadaka kwa watu waingiao ndani ya hekalu. Mtu huyu akiwaona Petro na Yohana wakiingia hekaluni aliomba apewe sadaka. Na Petro, akimkazia macho, pamoja na Yohana, akasema, Tutazame sisi. Akawaangalia, akitaraji kupata kitu kwao. Lakini Petro akasema, Mimi sina fedha, wala dhahabu, lakini nilicho nacho ndicho nikupacho. Kwa jina la Yesu Kristo wa Nazareti, simama uende. Akamshika mkono wa kuume, akamwinua, mara nyayo zake na vifundo vya miguu yake vikatiwa nguvu.”

 

-          Ulikuwa ni Muda ambao Kornelio  Mmataifa aliyekuwa anaomba na kutoa sana sadaka alipata utembeleo wa malaika akiagizwa na Mungu, kumuita Petro aje kumueleza habari za Kristo Matendo 10:1-6 “Palikuwa na mtu Kaisaria, jina lake Kornelio, akida wa kikosi kilichoitwa Kiitalia, mtu mtauwa, mchaji wa Mungu, yeye na nyumba yake yote, naye alikuwa akiwapa watu sadaka nyingi, na kumwomba Mungu daima. Akaona katika maono waziwazi, kama saa tisa ya mchana, malaika wa Mungu, akimjia na kumwambia, Kornelio! Akamtazama sana, akaogopa akasema, Kuna nini, Bwana? Akamwambia, Sala zako na sadaka zako zimefika juu na kuwa ukumbusho mbele za Mungu. Sasa basi, peleka watu Yafa, ukamwite Simoni, aitwaye Petro. Yeye ni mgeni wa mtu mmoja, jina lake Simoni, mtengenezaji wa ngozi, ambaye nyumba yake iko pwani, atakuambia yakupasayo kutenda.”

 

Hata saa tisa!

Luka 23:44-46. “Hapo ilikuwa yapata saa sita, kukawa giza juu ya nchi yote hata saa kenda, jua limepungua nuru yake; pazia la hekalu likapasuka katikati. Yesu akalia kwa sauti kuu, akasema, Ee Baba, mikononi mwako naiweka roho yangu

Nadhani sasa unaweza kuona umuhimu wa saa tisa, kimsingi ilikuwa ni Muda wa kutoa dhabihu ya jioni kwa wayahudi, ilikuwa ni saa ya kinabii, ulikuwa ni muda ambao wayahudi walipiga tarumbeta ya wito wa kwenda hekaluni kusali, Na Yesu yeye ndiye Dhabihu Halisi ya jioni, Alitumia Muda huo huo kukamilisha kazi yake ya ukombozi, Kristo alikuwa amekamilisha mpango wa Mungu wa kurudisha ushirika na wanadamu, ulikuwa ni muda ambao Msimamizi wa Mateso askari yule alimpiga Yesu Mkuki wa ubavuni ili kuthibitisha kama amekwisha kufa, ubavu ule ulitoa maji na damu, ambayo kimsingi ina thamani kubwa sana katika upatanisho wa watu kwa Mungu, Yesu alipewa Mkewe kutoka katika ubavu wake, (ni Kanisa) limezaliwa kutoka katoka moyo wa upendo wa Kristo, tunaona miujiza mingi, muda huo, tunaona watu wakijibiwa maombi muda huo, tunaona ni Muda ambao wayahudi hawakuomba sana walitumia muda mfupi tu, kwanini kwa sababu Mungu ni Mungu aliye karibu anapatikana na zaidi sana ulikuwa ni muda ambao wengi walitembelewa na malaika, kama muda wa usingizi kwa Adamu muda huo watu wengi waliofanya kazi kutwa nzima wanaweza kusinzia kidogo, ni Muda wa muujiza, ni muda wa rehema ni muda wa neema ya Mungu.

-          Mafunuo makubwa kuhusu Mungu yalishushwa saa tisa.

-          Utembeleo mkubwa wa malaika ulifanyika saa tisa.

-          Kupasuka kwa Pazia la Hekalu na watu wakaona patakatifu ilifanyika saa tisa.

-          Ulikuwa ni muda ambao wayahudi walitoa dhabihu ya pili ya mwanakondoo kwaajili ya upatanisho wa dhambi zao, na sasa tukio hilo la kinabii linakamilishwa na Bwana wetu Yesu

-          Dhabihu ya ukombozi wa mwanadamu ilikamilika saa tisa

-          Yesu alitundikwa Msalabani muda wa kutoa dhabihu ya asubuhi na alikufa muda wa kutoa dhabihu ya jioni

-          Ulikuwa muda wa Kujibiwa maombi kwa Eliya na Mungu alijibu kwa Moto.

-          Ulikuwa ni Muda wa Kujibiwa maombi Daniel kwa kutumiwa malaika

-          Ulikuwa ni Muda wa kutembelewa Abrahamu na wageni watatu

-          Ulikuwa Muda wa kufukiza uvumba katika madhabahu ya kufukiza uvumba wakati wa dhabihu ya jioni

-          Ulikuwa ni muda ambao malaika wa Bwana alimtokea Zekaria na kupewa ahadi ya kuzaliwa Yohana

-          Ulikuwa ni Muda wa kusali kwa Petro na Yohana na Muujiza mkubwa kwa kiwete wa miaka 40

-          Ulikuwa ni muda wa utembeleo kwa Kornelio kuona maono ya malaika

-          Miujiza mikubwa ya kubadilika kwa maisha ya watu ilitokea muda huo

-          Ulikuwa ni muda unaowakilisha saa ya kukubaliwa kwa maombi, Maandiko yanaonyesha hakuna mtu aliwahi kukataliwa kujibiwa maombi yake katika muda huo, japo Mungu anatusikia kila wakati.

-          Jambo kubwa la msingi na la Muhimu kuliko yote saa tisa ndio saa ya ukombozi wetu, kwani Yesu alikufa saa tisa na pazia la Hekalu lilipasuka kumpa kila mmoja nafasi ya kuweza kumfikia Mungu moja kwa moja kupitia sadaka iliyotolewa Msalabani na mwanaye Mpendwa, Yesu Kristo.

Saa tisa ilifanya kazi katika agano la kale na katika agano jipya, siwezi kukufundisha kuwa ufanye kitu saa tisa au uabudu saa tisa au uombe saa tisa,  lakini nataka kusema hivi, kila mtu anayeamini katika mateso, kufa na kufufuka kwa Bwana wetu Yesu na kuokolewa hapaswi kuwa gizani kuwa anapaswa kufanya nini muda huo na uzuri wake hauchukui muda mrefu, hivyo hata kama uko kazini, fanya kitu kidogo kwaajili ya Uhusiano wako na Mungu, Nyenyekea utaona miujiza mikubwa na utajua kwanini Yesu alikufa muda huo kifo kibaya sana kwaajili yetu, utajua kwanini pazia la hekalu lilipasuka, na patakatifu pakaonekana hii maana yake nini ni muda ambao unaweza kukikaribia kiti cha neema na kujipatia Rehema kutoka kwake aliyekuumba na nataka nikushuhudie ya kuwa utamuheshimu milele kwa sababu Bwana takupa neema ya kukusaidia wakati wa mahitaji yako, Kwa kweli saa tisa ni saa ambayo unaweza kuamuru muujiza wako, saa tisa ni kama saa ambayo Mungu yuko tayari kuamka na kufanya kitu kwaajili ya mwanadamu, ni saa ambayo tunaweza kusema Mzee hufungua ofisi yake ili asikilize watu wake, Hebu itumie saa hiii kwaajili ya kuamuru Baraka zako. neno hili ni kweli ni nani awezaye kulifahamu?

Waebrania 4:14-16 “Basi, iwapo tunaye kuhani mkuu aliyeingia katika mbingu, Yesu, Mwana wa Mungu, na tuyashike sana maungamo yetu. Kwa kuwa hamna kuhani mkuu asiyeweza kuchukuana nasi katika mambo yetu ya udhaifu; bali yeye alijaribiwa sawasawa na sisi katika mambo yote, bila kufanya dhambi. Basi na tukikaribie kiti cha neema kwa ujasiri, ili tupewe rehema, na kupata neema ya kutusaidia wakati wa mahitaji.”

 

Na. Rev. Innocent Samuel Kamote

Mkuu wa wajenzi mwenye Hekima       



Hakuna maoni: