Jumatatu, 29 Aprili 2024

Uamsho: Upendo wa Kwanza


Ufunuo 2:3-5 “tena ulikuwa na subira na kuvumilia kwa ajili ya jina langu, wala hukuchoka. Lakini nina neno juu yako, ya kwamba umeuacha upendo wako wa kwanza. Basi, kumbuka ni wapi ulikoanguka; ukatubu, ukayafanye matendo ya kwanza. Lakini, usipofanya hivyo, naja kwako, nami nitakiondoa kinara chako katika mahali pake, usipotubu.”



Utangulizi:

Nyakati hizi tulizo nazo ni nyakati za mwisho, maandiko yanasema mwisho wa mambo yote umekaribia 1Petro 4:7 “Lakini mwisho wa mambo yote umekaribia; basi, iweni na akili, mkeshe katika sala.” Katika nyakati hizi za mwisho nabiii nyingi zinazozungumziwa kama dalili za mwisho wa dunia zimekaribia,   Na ndio maana Petro anatukumbusha kuendelea kukesha yaani kudumu katika maombi, kuwa macho na kuongeza umakini. Moja ya unabii mkubwa unaoonyesha kuwa tuko katika wakati wa mwisho Yesu alisema licha ya kuongezeka kwa maasi lakini tunaelezwa kuwa Upendo wa wengi utapoa 

Mathayo 24:10-12 “Ndipo wengi watakapojikwaa, nao watasalitiana, na kuchukiana. Na manabii wengi wa uongo watatokea, na kudanganya wengi. Na kwa sababu ya kuongezeka maasi, upendo wa wengi utapoa.”

Upendo wa wengi kupoa pia ina maana ya kwamba kutokana na kuongezeka kwa maasi na uwepo wa manabii wengi wa uongo watu wengi watapoteza upendo wa kweli kwa Mungu na wanadamu, au tunaweza kusema upendo kwa Mungu na kwa kanisa lake, na matokeo yake ni kuwa katika nyakati hizi za mwisho ambazo shetani ataongeza kasi ya utendaji wake kazi, moja ya njia kubwa sana atakayo itumia ni kuhakikisha ya kuwa ile hamu na shauku ya kumuabudu Mungu na hata kumtumikia Mungu, kasi hiyo itapoa, na hapo ndipo tunaposema kuwa kanisa limepoa, au kanisa limelala au kanisa limekufa na linahitaji uamsho!

Kwa msingi huo basi katika somo hili lenye jina Uamsho: Upendo wa Kwanza tutachukua muda kujifunza na kutafakari kwa makini na kwa undani sana maswala yahusuyo uamsho na namna ya kuleta uamsho katika makanisa yetu; Bwana ampe neema kila mmoja wetu kufuatilia somo hili kwa umakini katika jina la Yesu Kristo Amen!, Tutajifunza somo hili kwa kuzingatia vipengele vitatu vifuatavyo:-


·         Maana ya Uamsho

·         Namna ya kujua kama unahitaji uamsho

·         Jinsi ya kurejesha uamsho


Maana ya Uamsho:

Kimsingi sio rahisi kupata neno uamsho moja kwa moja kutoka kwenye Biblia, lakini tunaweza kuliona neno uamsho katika namna isiyokuwa ya moja kwa moja kama tunavyoweza kuona katika mstari wetu wa Msingi ona

Ufunuo 2:3-5 “tena ulikuwa na subira na kuvumilia kwa ajili ya jina langu, wala hukuchoka. Lakini nina neno juu yako, ya kwamba umeuacha upendo wako wa kwanza. Basi, kumbuka ni wapi ulikoanguka; ukatubu, ukayafanye matendo ya kwanza. Lakini, usipofanya hivyo, naja kwako, nami nitakiondoa kinara chako katika mahali pake, usipotubu.”

Neno uamsho kibiblia linaweza kabisa kufananishwa na neno kuurudia upendo wa Kwanza, kama tunavyoweza kuona wito wa Bwana Yesu katika waraka wake kwa kanisa la Efeso kupitia Yohana katika kitabu cha ufunuo, Yesu aliliona Kanisa la Efeso kama Kanisa lililokuwa na uvumulivu, yaani subira, kwa ajili ya jina lake tena anawaona ya kuwa hawakuzimia moyo, lakini aliwaona pia kuwa upendo waliokuwa nao kwanza umepoa na ndio maana anawalaumu kuwa wameuacha upendo wa Kwanza, na kuwataka kufanya matendo yale ya kwanza, vinginevyo watapata adhabu! Wasipogeuka na kutubu, kihistoria kanisa la Efeso lilianza na wanafunzi 12 tu ambao kimsingi walikuwa hawajajazwa Roho Mtakatifu, na Paulo mtume alipofika hapo watu hao waliombewa na kumpokea Roho Mtakatifu, mahali hapo Mungu alimtumia Paulo mtume kwa miujiza mikubwa isiyohesabika, tena miujiza inayoitwa ya kupita kawaida, watu waliokolewa kwa wingi katika mji huu na watu waliotumia mambo ya uchawi na uganga walichoma vitabu vyao kukawa na uamsho mkubwa sana jina la Yesu likatukuzwa

Matendo 19:1-7 “Ikawa, Apolo alipokuwa Korintho, Paulo, akiisha kupita kati ya nchi za juu, akafika Efeso; akakutana na wanafunzi kadha wa kadha huko; akawauliza, Je! Mlipokea Roho Mtakatifu mlipoamini? Wakamjibu, La, hata kusikia kwamba kuna Roho Mtakatifu hatukusikia. Akawauliza, Basi mlibatizwa kwa ubatizo gani? Wakasema, Kwa ubatizo wa Yohana. Paulo akasema, Yohana alibatiza kwa ubatizo wa toba, akiwaambia watu wamwamini yeye atakayekuja nyuma yake, yaani, Yesu. Waliposikia haya wakabatizwa kwa jina la Bwana Yesu. Na Paulo, alipokwisha kuweka mikono yake juu yao, Roho Mtakatifu akaja juu yao; wakaanza kunena kwa lugha, na kutabiri. Na jumla yao walipata wanaume kumi na wawili.”

Matendo 19:11-12 “Mungu akafanya kwa mikono ya Paulo miujiza ya kupita kawaida; hata wagonjwa wakaletewa leso na nguo zilizotoka mwilini mwake, magonjwa yao yakawaondokea, pepo wachafu wakawatoka.”

Matendo 19:17-20 “Habari hii ikajulikana na Wayahudi wote na Wayunani waliokaa Efeso, hofu ikawaingia wote, na jina la Bwana Yesu likatukuzwa. Na wengi wa wale walioamini wakaja wakaungama, wakidhihirisha matendo yao. Na watu wengi katika wale waliotumia mambo ya uganga wakakusanya vitabu vyao, wakavichoma moto mbele ya watu wote; wakafanya hesabu ya thamani yake, wakaona ya kwamba yapata fedha hamsini elfu. Hivyo ndivyo neno la Bwana lilivyozidi na kushinda kwa nguvu.”

Unapoyaangalia maandiko hayo yanakuonyesha wazi kuwa Kanisa la Efeso lilikuwa ni moja ya Kanisa lenye nguvu kubwa sana, watu walijazwa Roho Mtakatifu, miujiza ya kupita kawaida ilitendeka, hofu ya Mungu iliushika mji mzima neno la Mungu lilipata nguvu, Kanisa la Efeso lilianzishwa katika mwaka wa 52-54 AD Baada ya Kristo, Lakini unaweza kuona kuwa wakati Yesu anawaandikia waraka katika mwaka wa 95-100 AD ni muda wa miaka kama 40 hivi au 41 Kanisa lilikuwa tayari limepoteza hali yake ya kwanza, yaani limeuacha upendo wa kwanza na Yesu analiita kutubu, kanisa lilikuwa limepoa, kanisa lilikuwa limelala kanisa lilikuwa linahitaji uamsho! Je Kanisa lenu lina miaka mingapi sasa? Kama nyakati za kanisa la kwanza miaka 40 tu watu walikuwa wameanza kupoa je kanisa lenu linahitaji miaka mingapi sasa ili mjue ya kuwa limepoa? Baki na jibu lako moyoni!  Je ni vibaya kuliamsha? je huoni ya kuwa mnahitaji uamsho? Uamsho ni nini Hasa?

-          Neno uamsho  kwa kiingereza linatumika neno REVIVAL ambalo tafasiri yake kwa kiingereza ni Restoration to life, consciousness, vigor, strength  au awakening in the church or community of interest and care for matters relating to Personal religion

-          Kwa hiyo Uamsho kurejesha kwenye uhai, kufufua, dhamiri, au kuamsha nia ya mtu asiyejitambua ajitambue, au kurejesha nguvu zilizopungua au kupotea

-          Uamsho ni kufufua Habakuki 3:2 “Ee Bwana, nimesikia habari zako, nami naogopa; Ee Bwana, fufua kazi yako katikati ya miaka; Katikati ya miaka tangaza habari yake; Katika ghadhabu kumbuka rehema.” Neno la kiingereza linalotumika kuhusu Fufua ni neno REVIVE katika kiebrania neno hilo linasomeka kama CHAYAH  (  חיק    ) ambalo maana yeke ni REPAIR   sawa na neno UKARABATI katika Kiswahili au kuhuhisha

-          Yesu anatumia neno kurejesha upendo wa kwanza, hii maana yake ni nini hasa?

Wengi wetu tulipompokea Yesu kwa mara ya kwanza, tulijawa na furaha kubwa sana, tulijisikia huru, tulijiona wepesi ni kama Yesu ameondoa mizigo Fulani iliyokuwa inatuelemea, tulijawa na upendo mkubwa sana kwa Mungu na tulihisi kuwa tuko karibu sana na Yesu! Mioyo yetu ilijawa na kiu na  hamu na shauku, ya kutaka kumtumikia Mungu, tulisoma neno la Mungu kwa nguvu na mioyo yetu yote, tulihudhuria ibada bila kukosa huku tukitoa kipaumbele kwa ibada kuliko kitu kingine, tulikuwa waombaji, tulihudhuria mikesha, tulishuhudia habari njema na kuwaleta wengi kwa Yesu, tulikuwa na mijadala ya kidini na ndugu na jamaa zetu,  hatukuweza kutulia, tulijawa na wivu kwa ajili ya Mungu, tulifuatilia watoto wachanga kiroho, tulitembelea magerezani, mahospitalini, wagonjwa, yatima na wajane, tulijali mambo ya Mungu, tulitoa bila kusukumwa, hata ndoto na maono yetu yalikuwa ya kimbingu,  maisha na mwenendo wetu haukuwa na mashaka watu walikuwa na kiu na hamu na shauku ya kuwa kama Yesu Kristo!, Nyimbo zetu zilikuwa nataka kuwa kama Yesu moyo wangu, nataka kuwa kama Yesu maisha yangu!  Hali hii ndio inaitwa upendo wa Kwanza, ni kama Uchumba au ndoa inavyokuwa mwanzoni, kila mmoja anavyojitoa kwa mpenzi wake hali hiyo ndiyo inaitwa upendo wa Kwanza! Kila mmoja wetu alikuwa nayo, na makanisa yetu mengi yalikuwa hivyo, Pepo walikuwa wakiwatoka watu wenyewe wakati wa kusifu, au hata kwa kuwepo tu kanisani, kabla hata ya kukemea kwa nguvu udhihirisho wa Mungu ulikuwa ni kitu cha wazi wazi! huo ndio, watu walikuwa na kiu ya kutenda haki, hakukuwa na majivuno, hakukuwa na kiburi, hakukuwa na ukaidi, utii ulikuwa wa hali ya juu, hakukuwa na upendeleo makanisani, hakukuwa na ukabila, hakukuwa na ugomvi wala mafarakano, hakukuwa na kupindishwa kwa haki, wala dhuluma, wala wivu, wala kubaniana, wala hakukuwa na urasimu, Mungu alikuwa akisema wazi wazi na watu wake hata kwa unabii, karama za Roho Mtakatifu zilidhihirika!  Je mambo hayo yapo? Wakati huo hakukutumika sana mafuta wala visaidizi vya kiroho, hatukujua chumvi, wala maji ya Baraka (sisemi kwamba kutumia vifaa vya kiroho ni vibaya) lakini visaidizi vya kiroho hutumiwa na watu ambao Imani imeshuka sana yaani wenye Imani ya kawaida kwaajili ya kuinua Imani zao, Wakati wa uamsho mkubwa sisi tulilijua jina la Yesu tu! Huo ndio uamsho!  Jina la Yesu lilikuwa ni utoshelevu mkubwa kwa kutamka tu  wakati wa uamsho watu walifanya maamuzi magumu,Watu waliacha kazi Redioni, ili tu wasipige miziki isiyompendeza Mungu, watu walifunga baa zao, watu waliacha kuuza sigara huo ndio ulikuwa uamsho!  Watu waliuza nyumba zao na mali zao kwaajili ya injili, Watu walikuwa wakiokolewa na wokovu ulikuwa una vita kali sana katika ngazi za familia na jamii, watu walikuwa na msimamo mkali hiyo ndio ilikuwa hali ya uamsho, watu walijitenga na dunia wala hawakufuatisha namna ya dunia hii katika usemi, menendo Imani na ufasi, haki ilitendeka kila mahali watumishi walizaa watumishi, watu walikuwa kiroho kwa haraka, kazi ya Mungu ilisonga mbele na Mungu alidhihirika wazi wazi kati ya watu wake!

Ni Muhimu kufahamu kuwa Kanisa linapokuwa na nguvu kubwa namna hii, maana yake ufalme wa Shetani unapata taabu sana, na shetani hawezi kukubali kirahisi ashambuliwe na watu wake kuchukuliwa mateka kwenda upande wa  ufalme wa Mungu, na ndio maana mara baada ya mtu kuokolewa yeye anaanza kuwa na mipango mikakati ya kuhakikisha kuwa anawarejesha nyuma au katika ufalme wake wale wote ambao wametekwa kwenda upande wa ufalme wa Mungu, shetani anajua wazi kuwa ni kazi ngumu kuwarejesha mateka wake katika mikono ya Mungu

Yohana 10:27-29 “Kondoo wangu waisikia sauti yangu; nami nawajua, nao wanifuata. Nami nawapa uzima wa milele; wala hawatapotea kamwe; wala hakuna mtu atakayewapokonya katika mkono wangu. Baba yangu aliyenipa hao ni mkuu kuliko wote; wala hakuna mtu awezaye kuwapokonya katika mkono wa Baba yangu.”

Kwa hiyo mbinu kubwa anayoitumia shetani ni kuhakikisha kuwa watu wa Mungu wanapoa, wanakinai, wanachoka, wanapoteza tumaini, wanakosa upendo, shauku na hamu ya kumpenda Yesu, Shetani hatakurudisha nyuma kwenye dini yako ya zamani, lakini anakufanya usiwe na madhara katika ufalme wake huku ukiwa katika ufalme wa Mungu,  atahakikisha kuwa unabaki kama Mtumishi au Mkristo asiye tishio katika ufalme wa ibilisi, hutaomba tena, hutakuwa mshabiki wa mikesha, huoni umuhimu wa kuhudhuria ibada husikilizi nyimbo za injili tena na huna madhara kwa wasiookoka wala kwa shetani mwenyewe huko ndiko kuuacha upendo wako wa kwanza ndio kupoa! Atakuacha shetani uwe vuguvugu, atakuacha ufungiwe nira na wasiamini, atakuacha uwe na urafiki na giza, atakuacha uipende dunia, haijalishi uko katika kanisa gani wala haijalishi kuwa uko na mtumishi wa kiwango gani cha kiroho utapoa tu

2Timotheo 4: 9-10 “Jitahidi kuja kwangu upesi. Maana Dema aliniacha, akiupenda ulimwengu huu wa sasa, akasafiri kwenda Thesalonike; Kreske amekwenda Galatia; Tito amekwenda Dalmatia.”                 

Kwa msingi huo ni muhimu kila mtu na kila kanisa kujihoji na kujiuliza kama wako salama au la? Na ni vigumu sana kwa kanisa au mkristo aliyepoa kukubali kuwa amepoa au amekufa kiroho, lakini swala la msingi la kujiuliza ni je bado tunampenda Yesu kwa kiwango kile kile?, je tunatafuta ufalme wa Mungu kwanza na haki yake? Je tuna upendo wa kweli na ushirika wa kweli kwa na ndugu zetu katika Bwana? Je tunashuhudia matunda ya Roho katika maisha ya wakristo na watumishi wa Mungu leo? je ziko nguvu za Mungu katika maisha yetu na kanisa letu?, Leo hii imefikia hatua hata wachwi wanaabudu katika makanisa ya kiroho, watu wa Mungu pia wanarogwa! Niliwahi kumsikia Mchungaji mmoja akilalamika kuwa wachawi wanakopera sadaka katika Kanisa Lake! Mpaka aliposimama na kukemea kwa midomo yake kuwa waache tabia hizo ndio sadaka zikaongezeka! Sikumjibu lolote nilikuwa na mke wangu hakua aliyesema kitu pale lakini tulipofika nyumbani tulianza kujiuliza, kama Askofu yule angeliruambia sadaka zinaibiwa angalau akili yangu ingeweza kuwa na Amani, kwamba wako wezi ambao hawana hofu ya Mungu wameingia makanisani, lakini hebu fikiria wachawi wanakopera sadaka katika kanisa la kiroho? Ni jambo la kusikitisha sana, ni lazima kanisa lirejee, lirudi mahali pake mahali ambapo limejengwa na malango ya kuzimu hayataliweza! Na msingi huo ni Yesu Kristo Mwana wa Mungu aliye hai!, Je hali ya kanisa lenu wewe na hali yakow ewe mwenyewe na hali ya wenzako na zamani zile ikoje? Yako makanisa ukiokoka leo na ukawa wa moto sana wenzako waliokutangulia utasikia kaka ana moto sana dada ana moto sana aaa ni uchanga tu atapoa sasa hivi Je umewahi kusikia hali kama hiyo?

Marko 12:30 “nawe mpende Bwana Mungu wako kwa moyo wako wote, na kwa roho yako yote, na kwa akili zako zote, na kwa nguvu zako zote.”

Mathayo 6:33 “Bali utafuteni kwanza ufalme wake, na haki yake; na hayo yote mtazidishiwa.”

1Yohana 1:7 “bali tukienenda nuruni, kama yeye alivyo katika nuru, twashirikiana sisi kwa sisi, na damu yake Yesu, Mwana wake, yatusafisha dhambi yote.”

1Yohana 4:20-21 “Mtu akisema, Nampenda Mungu, naye anamchukia ndugu yake, ni mwongo; kwa maana asiyempenda ndugu yake ambaye amemwona, hawezi kumpenda Mungu ambaye hakumwona. Na amri hii tumepewa na yeye, ya kwamba yeye ampendaye Mungu, ampende na ndugu yake.”

Wagalatia 5:22-23 “Lakini tunda la Roho ni upendo, furaha, amani, uvumilivu, utu wema, fadhili, uaminifu, upole, kiasi; juu ya mambo kama hayo hakuna sheria.”

Matendo 1:8 “Lakini mtapokea nguvu, akiisha kuwajilia juu yenu Roho Mtakatifu; nanyi mtakuwa mashahidi wangu katika Yerusalemu, na katika Uyahudi wote, na Samaria, na hata mwisho wa nchi.”

Kama maswali yote tuliyojiuliza hapo juu yanatoa jibu hapana au kuna upungufu basi ukweli ni kuwa tunahitaji uamsho! au kwa lugha nyingine ni kuwa tumepoa au kanisa lisilo na hayo au lenye mapoungufu kuhusu hayo limepoa limekuwa la baridi na sio la moto tena moto umezimika au moto umefifia kwa hiyo tunahitaji uamsho!       

Namna ya kujua kama unahitaji uamsho;

Ni vigumu watu, mtu au kanisa lolote lile kukubali kuwa limelala, au limepoa na linahitaji uamsho lakini ni rahisi kujijua kama tuna uamsho au la kwa kujiuliza maswali kadhaa Muhimu, maandiko hayakatazi kujitathimini, na kujijaribu wenyewe ili kujua kama tumekuwa katika Imani au lahasha

2Wakorintho 13:5 “Jijaribuni wenyewe kwamba mmekuwa katika imani; jithibitisheni wenyewe. Au hamjijui wenyewe, kwamba Yesu Kristo yu ndani yenu? Isipokuwa mmekataliwa.”

Tunawezaje kujua kama tuko vema au la Maswali kadhaa yajayo yatasaidia kujitambua tuko hai kiasi gani au tuko hoi kiasi gani

1.       Je tunampenda Mungu kuliko Kazi zetu, familia zetu, biashara zetu, anasa zetu na mambo yetu?  Mathayo 6:33 “Bali utafuteni kwanza ufalme wake, na haki yake; na hayo yote mtazidishiwa.

 

2.       Kumnung’unikia Mungu na watumishi wake katika kila hali unayokutana nayo katika maisha 1Wakorintho 10:10 “Wala msinung'unike, kama wengine wao walivyonung'unika, wakaharibiwa na mharabu.”

 

3.       Tunapenda sifa za wanadamu? Tunapenda kusifiwa kwa kila tendo jema?, tunapenda kutukuzwa sisi kuliko Kristo? Yohana 12:42-43 “Walakini hata katika wakuu walikuwamo wengi waliomwamini; lakini kwa sababu ya Mafarisayo hawakumkiri, wasije wakatengwa na sinagogi. Kwa maana walipenda utukufu wa wanadamu kuliko utukufu wa Mungu.”

 

4.       Kuwa na uchungu, kukosa uvumilivu kwa wengine, kukosoa wengine, kuwa mkali sana ukikosolewa, wivu kwa wengine na kutokutaka mafanikio ya wengine, kukomoa wengine na kufurahia tunapoona wanaharibikiwa?  Waebrania 12:14-15 “Tafuteni kwa bidii kuwa na amani na watu wote, na huo utakatifu, ambao hapana mtu atakayemwona Bwana asipokuwa nao; mkiangalia sana mtu asiipungukie neema ya Mungu; shina la uchungu lisije likachipuka na kuwasumbua, na watu wengi wakatiwa unajisi kwa hilo.”

 

5.       Kukwaza wengine, kupenda mabishano, kujiona uko sawa wakati wote, mkali sana kwa wengine, kujisikia vibaya wengine wakifanikiwa, kuogopa watu watasemaje, kufurahia watu wengine wanapokwama, au kuanguka, kukosa kabisa matunda ya roho na kujaa matunda ya mwili, kutokusemeshana, dhuluma, majungu, hila, fitina, uzushi, husuda yaani ni matunda ya mwili tupu, Wagalatia 5:19-21 “Basi matendo ya mwili ni dhahiri, ndiyo haya, uasherati, uchafu, ufisadi, ibada ya sanamu, uchawi, uadui, ugomvi, wivu, hasira, fitina, faraka, uzushi, husuda, ulevi, ulafi, na mambo yanayofanana na hayo, katika hayo nawaambia mapema, kama nilivyokwisha kuwaambia, ya kwamba watu watendao mambo ya jinsi hiyo hawataurithi ufalme wa Mungu.

 

6.       Kukosa uaminifu, kutokuwa mkweli, kusema uongo, kuficha maovu, kujitahidi kujipa raha ili hali huna raha, wala Amani, kuishi maisha ya kinafiki, kuwa na sura mbilimbili, Mathayo 23:27-28 “Ole wenu, waandishi na Mafarisayo, wanafiki! Kwa kuwa mmefanana na makaburi yaliyopakwa chokaa, nayo kwa nje yaonekana kuwa mazuri, bali ndani yamejaa mifupa ya wafu, na uchafu wote. Vivyo hivyo ninyi nanyi, kwa nje mwaonekana na watu kuwa wenye haki, bali ndani mmejaa unafiki na maasi.”         

 

7.       Kusumbuliwa na mawazo, mgandamizo wa mawazo, kukata tamaa na kuacha kumtumaini Mungu Waebrania 11:6 “Lakini pasipo imani haiwezekani kumpendeza; kwa maana mtu amwendeaye Mungu lazima aamini kwamba yeye yuko, na kwamba huwapa thawabu wale wamtafutao.”   

 

8.       Kuwa wakavu kiroho, kuwa wa kawaida sana, kutokushuhudia, kutokufanya uinjilisti, kuwa dhaifu kiroho, kuwa vugu vugu, kurudi nyuma Ufunuo 2:4-5 “Lakini nina neno juu yako, ya kwamba umeuacha upendo wako wa kwanza. Basi, kumbuka ni wapi ulikoanguka; ukatubu, ukayafanye matendo ya kwanza. Lakini, usipofanya hivyo, naja kwako, nami nitakiondoa kinara chako katika mahali pake, usipotubu.”

               

Ufunuo 3:15-16“Nayajua matendo yako, ya kuwa hu baridi wala hu moto; ingekuwa heri kama ungekuwa baridi au moto. Basi, kwa sababu una uvuguvugu, wala hu baridi wala moto, nitakutapika utoke katika kinywa changu.”

 

9.        Kuanza kuifuatisha namna ya dunia hii, kuupenda ulimwengu, kuanza kufikiri, kusema na kutenda kama watu wa ulimwengu huu tu Warumi 12:1-2 Basi, ndugu zangu, nawasihi, kwa huruma zake Mungu, itoeni miili yenu iwe dhabihu iliyo hai, takatifu, ya kumpendeza Mungu, ndiyo ibada yenu yenye maana. Wala msiifuatishe namna ya dunia hii; bali mgeuzwe kwa kufanywa upya nia zenu, mpate kujua hakika mapenzi ya Mungu yaliyo mema, ya kumpendeza, na ukamilifu.”       

 

10.   Kuacha kuomba, kuacha kushuhuhudia, kuacha kuhubiri injili, kuacha kuhudhuria ibada, kuacha kujali waliorudi nyuma, kuacha kusoma neno, kupuuzia karama za roho, kutweza unabii, kuwasumbua wenye vipawa badala ya kuwalea, kuacha kufundisha neno la Mungu, kuhubiri mafanikio ya mwilini zaidi kuliko maswala ya rohoni, na mkazo wa matumizi ya vifaa vya kiroho zaidi kuliko jina la Yesu, kukatisha tamaa watu wenye bidi katika bwana, kuwabania watumishi wa Mungu wenye vipawa, kumzimisha Roho Mtakatifu 1Wathesalonike 5:19 “Msimzimishe Roho

 

11.   Kurudi kwa magonjwa mbalimbali makubwa ambayo zamani yalikuwa yakiwasumbua watu wa dunia hii Kutoka 23:25-27 “Nanyi mtamtumikia BWANA, Mungu wenu, naye atakibarikia chakula chako, na maji yako; nami nitakuondolea ugonjwa kati yako. Hapatakuwa na mwenye kuharibu mimba, wala aliye tasa, katika nchi yako; na hesabu ya siku zako nitaitimiza. Nitatuma utisho wangu utangulie mbele yako, nami nitawafadhaisha watu wote utakaowafikilia, nami nitawafanya hao adui zako wote wakuonyeshe maungo yao.”    

 

12.   Endapo utaanza kuona uovu na uharibifu Habakuki 1:2-4 “Ee Bwana, nilie hata lini, wewe usitake kusikia? Nakulilia kwa sababu ya udhalimu, ila hutaki kuokoa. Mbona wanionyesha uovu, na kunitazamisha ukaidi? Maana uharibifu na udhalimu u mbele yangu; kuna ugomvi, na mashindano yatokea. Kwa sababu hiyo sheria imelegea, wala hukumu haipatikani; kwa maana watu wabaya huwazunguka wenye haki; kwa sababu hiyo hukumu ikipatikana imepotoka.”             

 

Endapo kila mmoja na kila kanisa litajifanyia tathimini na kujichunguza kuona mapungufu yetu ukilinganisha na jinsi tulivyoanza wakati tunakutana na Yesu na tukibaini kuwa kuna mapungufu, basi mara moja tunaweza kufahamu kuwa tunahitaji uamsho bwana ampe neema kila mmoja wetu kuwa na ufahamu na kuanza kuutafuta uamsho katika maisha yetu katika jina la Yesu Kristo.

 

Jinsi ya kurejesha uamsho

Uamsho ni kurejesha upendo, ule upendo wetu wa kwanza tuliokuwa nao kwa Yesu Kristo,  ni kurejea katika kila jambo ambalo tuliliacha na ambalo limeagizwa katika neno la Mungu, ni kurejesha afya ya kiroho ambayo imepungua katika maisha yetu na katika kanisa, na jambo la kwanza ambalo tunaweza kuanza nalo ni toba, na kuomba rehema za Mungu,  ujumbe wa toba hauna uhusiano na watu walioko nje, watu ambao hawajaokolewa ujumbe wao ni habari njema ya kuwa Yesu Kristo anaokoa, na hivyo wanapaswa kumuamini na kukubali kazi yake aliyoifanya msalabani kwaajili ya ulimwengu mzima, ujumbe wa toba ni ujumbe kwa kanisa  ni ujumbe kwa watu wa Mungu, wanaoambiwa watubu ni makanisa ni watu ambao walimjua Mungu na kisha wakaingia kwenye njia mbaya kwa hiyo unatolewa wito kwao kumrudia Bwana  na Mungu takapoona mioyo yetu iko tayari yeye ndiye anayeleta uamsho, bidi na jitihada za kibinadamu kamwe haziwezi kuleta uamsho!

Mathayo 26:40-43 “Akawajia wale wanafunzi, akawakuta wamelala, akamwambia Petro, Je! Hamkuweza kukesha pamoja nami hata saa moja? Kesheni, mwombe, msije mkaingia majaribuni; roho i radhi, lakini mwili ni dhaifu.Akaenda tena mara ya pili, akaomba, akisema, Baba yangu, ikiwa haiwezekani kikombe hiki kiniepuke nisipokunywa, mapenzi yako yatimizwe. Akaja tena, akawakuta wamelala; maana macho yao yamekuwa mazito.”

Wakati wote wanafunzi walipokuwa wamelala ni Yesu ndiye aliyewaamsha, umasho hauwezi kuletwa na mwanadamu mwenyewe, yako maandalizi ya kawaida ya kufanya lakini mwenye kuamsha hiyo nia na hiyo hari ni Mungu mwenyewe kumbuka yale maombi ya nabii Habakuki. Habakuki 3:2 “Ee Bwana, nimesikia habari zako, nami naogopa; Ee Bwana, fufua kazi yako katikati ya miaka; Katikati ya miaka tangaza habari yake; Katika ghadhabu kumbuka rehema.” Hata hivyo kama wanadamu tuna wajibu wa kufanya sehemu yetu na haya ndio tunayoweza kuyafanya!

Toba:

Ufunuo 2: 4-6 “Lakini nina neno juu yako, ya kwamba umeuacha upendo wako wa kwanza. Basi, kumbuka ni wapi ulikoanguka; ukatubu, ukayafanye matendo ya kwanza. Lakini, usipofanya hivyo, naja kwako, nami nitakiondoa kinara chako katika mahali pake, usipotubu. Lakini unalo neno hili, kwamba wayachukia matendo ya Wanikolai, ambayo na mimi nayachukia

Ufunuo 2:14-16 “Lakini ninayo maneno machache juu yako, kwa kuwa unao huko watu washikao mafundisho ya Balaamu, yeye aliyemfundisha Balaki atie ukwazo mbele ya Waisraeli, kwamba wavile vitu vilivyotolewa sadaka kwa sanamu, na kuzini. Vivyo hivyo wewe nawe unao watu wayashikao mafundisho ya Wanikolai vile vile. Basi tubu; na usipotubu, naja kwako upesi, nami nitafanya vita juu yao kwa huo upanga wa kinywa changu.”

2Nyakati 7:14 “ikiwa watu wangu, walioitwa kwa jina langu, watajinyenyekesha, na kuomba, na kunitafuta uso, na kuziacha njia zao mbaya; basi, nitasikia toka mbinguni, na kuwasamehe dhambi yao, na kuiponya nchi yao.”

Marekebisho:

Toba haiwezi kuwa kamili bila kufanya marekebisho, au matengenezo, hatuna budi kuhakikisha kuwa tunaweka sawa pale ambapo tuliharibu, mfano kama ulidhulumu watu umetubu na watu hao wapo uerejeshe kile ulichodhulumu, uliazima vitabu Library (maktaba ya shule) na hujavirudisha rejesha, una mume ambaye si wako, au mke ambaye si wako mwachie aende kwa mmewe au mkewe,  swala la toba na malipizo katika makanisa mengi linachukuliwa poa, lakini ni fundisho halali na liko, umemkosea mtu usijikaushe tu nenda kaombe msamaha,  Kumbuka jinsi Yakobo alivyotafuta Amani kwa bidi kwa kaka yake Esau!, hakikisha hauna mtu moyoni mwako samehe, sahau achilia.

Mathayo 5:23-24 “Basi ukileta sadaka yako madhabahuni, na huku ukikumbuka ya kuwa ndugu yako ana neno juu yako, iache sadaka yako mbele ya madhabahu, uende zako, upatane kwanza na ndugu yako, kisha urudi uitoe sadaka yako.”

Luka 19:8-9 “Zakayo akasimama, akamwambia Bwana, Tazama, Bwana, nusu ya mali yangu nawapa maskini, na ikiwa nimenyang'anya mtu kitu kwa hila namrudishia mara nne.Yesu akamwambia, Leo wokovu umefika nyumbani humu, kwa sababu huyu naye ni mwana wa Ibrahimu.”

Ezra 10:1-3 “Basi hapo Ezra alipokuwa akiomba na kuungama, akilia, na kujiangusha kifudifudi mbele ya nyumba ya Mungu, wakamkusanyikia katika Israeli wote kusanyiko kubwa sana la wanaume, na wanawake, na watoto; maana watu hao walikuwa wakilia sana. Hata Shekania, mwana wa Yehieli, mmoja wa wana wa Elamu, akajibu, akamwambia Ezra, Sisi tumemkosa Mungu wetu, nasi tumeoa wanawake wageni wa watu wa nchi hizi; lakini kungaliko tumaini kwa Israeli katika jambo hili. Haya basi! Na tufanye agano na Mungu wetu, kuachana na wake zetu, na wale waliozaliwa nao, tukilifuata shauri la bwana wangu, na shauri la hao wanaoitetemekea amri ya Mungu wetu; mambo haya na yatendeke kwa kuifuata torati.”

Waebrania 12:14 “Tafuteni kwa bidii kuwa na amani na watu wote, na huo utakatifu, ambao hapana mtu atakayemwona Bwana asipokuwa nao;”

Maombi:

Maombi ni funguo muhimu sana katika kutafuta uamsho wa katika kanisa, unaposoma vitabu vingi sana vuinavyozungumzia uamsho huwezi kuona kuna mwandishi amewahi kuacha kuzungumzia maombi kuwa ni moja wapo ya nyenzo muhimu sana katika kuleta uamsho, ndio njia ya Imani, unyenyekevu, na yenye kuchochea mabadiliko, Mungu anatutegemea tumuombe ili aweze kuleta Baraka zake kwetu kwa mtu mmoja mmoja na kanisa zima kwa ujumla, maombi hayo ndiyo yanayohusisha toba,  na kutafuta rehema, na kutimiza kiu yetu ya kukleta uamsho, tunaweza kumuomba Mungu aokoe wengine, kuombea umisheni na uinjilisti, kuhitaji uwepo wa Mungu, karama na vipawa, nguvu za Roho Mtakatifu na mpenyo wa kiroho maombi maombi maombi

Matendo 1:12-14 “Kisha wakarudi kwenda Yerusalemu kutoka mlima ulioitwa wa Mizeituni, ulio karibu na Yerusalemu, wapata mwendo wa sabato. Hata walipoingia, wakapanda orofani, walipokuwa wakikaa; Petro, na Yohana, na Yakobo, na Andrea, Filipo na Tomaso, Bartholomayo na Mathayo, Yakobo wa Alfayo, na Simoni Zelote, na Yuda wa Yakobo.Hawa wote walikuwa wakidumu kwa moyo mmoja katika kusali, pamoja nao wanawake, na Mariamu mama yake Yesu, na ndugu zake.”    

Kufunga:

Kufunga ni njia ya kujitia nidhamu ya kiroho kwa kusudi la kujiungamanisha na Mungu, kumlingana Mungu, kuutafuta uso wake kwa bidii ili kwamba Mungu aweze kuingilia kati na kuleta badiliko tunalolikusudia, Kufunga kunaongezea nia yetu ya kuonyesha kuwa tunamtafuta Mungu kwa bidi hii ni kwa sababu kufunga huambatana na kuomba, kuomba kunajumuisha unyenyekevu, tafakari, na kutafuta mpenyo wa kirohoni nyenzo muhimu, yasiyowezekana katika hali ya kawaida yanaweza kusawazishwa kwa maombi ya kufunga, kufunga kufunga. Kufunga kulitumika kama njia ya kuonyesha kujidhabihu kama ibada ya kuutafuta uso wa Mungu lakini pia kwaajili au ikama njia ya kumrudia Bwana

Yoeli 2:12-14 “Lakini hata sasa, asema Bwana, nirudieni mimi kwa mioyo yenu yote, na kwa kufunga, na kwa kulia, na kwa kuombolea; rarueni mioyo yenu, wala si mavazi yenu, mkamrudie Bwana, Mungu wenu; kwa maana yeye ndiye mwenye neema, amejaa huruma; si mwepesi wa hasira, ni mwingi wa rehema, naye hughairi mabaya. N'nani ajuaye kwamba hatarudi na kugeuka, na kutuachia baraka nyuma yake, naam, sadaka ya unga, na sadaka ya kinywaji, kwa Bwana, Mungu wenu?              

Matendo 13:1-3 “Na huko Antiokia katika kanisa lililokuwako palikuwa na manabii na waalimu, nao ni Barnaba, na Simeoni aitwaye Nigeri, na Lukio Mkirene, na Manaeni aliyekuwa ndugu wa kunyonya wa mfalme Herode, na Sauli. Basi hawa walipokuwa wakimfanyia Bwana ibada na kufunga, Roho Mtakatifu akasema, Nitengeeni Barnaba na Sauli kwa kazi ile niliyowaitia. Ndipo wakiisha kufunga na kuomba, wakaweka mikono yao juu yao, wakawaacha waende zao.”

 

Unyenyekevu:  watu wengi sana hawafahamu siri ya kuinuliwa na Mungu, Mungu anapendezwa sana na watu wanyenyekevu, anakaa yeye na watu wanyenyekevu na waliotubu, moja ya sababu ya watu wengi kuachwa na Mungu ni kwa sababu ya kiburi na majivuno, siku hizi hata makanisa ya kipentekoste wachungaji wanaitwa Baba! Na watu wanaona ni jambo la kawaida tu wala hawalikemei, Mungu hakai na watu wenye kiburi, watu wanaojifikiri kuwa bora zaidi kuliko wengine, na hata kujikinai wakiwadharau wengine kama tunataka uwepo wa Mungu na kukubaliwa na Mungu hatuna budi kuweka mbali kiburi na majivuno, na wakati wote tukiri ya kuwa tunahitaji neema ya Mungu

Isaya 66:2 “Maana mkono wangu ndio uliofanya hivi vyote, vitu hivi vyote vikapata kutokea, asema Bwana; lakini mtu huyu ndiye nitakayemwangalia, mtu aliye mnyonge, mwenye roho iliyopondeka, atetemekaye asikiapo neno langu.”                

1Petro 5:5-6 “Vivyo hivyo ninyi vijana, watiini wazee. Naam, ninyi nyote jifungeni unyenyekevu, mpate kuhudumiana; kwa sababu Mungu huwapinga wenye kiburi, lakini huwapa wanyenyekevu neema. Basi nyenyekeeni chini ya mkono wa Mungu ulio hodari, ili awakweze kwa wakati wake

Yakobo 4:5-6 “Lakini hutujalia sisi neema iliyozidi; kwa hiyo husema, Mungu huwapinga wajikuzao, bali huwapa neema wanyenyekevu.”

Luka 18:10-14 “Watu wawili walipanda kwenda hekaluni kusali, mmoja Farisayo, wa pili mtoza ushuru. Yule Farisayo akasimama akiomba hivi moyoni mwake; Ee Mungu, nakushukuru kwa kuwa mimi si kama watu wengine, wanyang'anyi, wadhalimu, wazinzi, wala kama huyu mtoza ushuru. Mimi nafunga mara mbili kwa juma; hutoa zaka katika mapato yangu yote. Lakini yule mtoza ushuru alisimama mbali, wala hakuthubutu hata kuinua macho yake mbinguni, bali alijipiga-piga kifua akisema, Ee Mungu, uniwie radhi mimi mwenye dhambi. Nawaambia, huyu alishuka kwenda nyumbani kwake amehesabiwa haki kuliko yule; kwa maana kila ajikwezaye atadhiliwa, naye ajidhiliye atakwezwa.”

2Nyakati 7:14 “ikiwa watu wangu, walioitwa kwa jina langu, WATAJINYENYEKESHA, na kuomba, na kunitafuta uso, na kuziacha njia zao mbaya; basi, nitasikia toka mbinguni, na kuwasamehe dhambi yao, na kuiponya nchi yao.”

Neno la Mungu:

Neno la Mungu ndio kiini kikuu cha uamsho, lenyewe ndilo ambalo hutumika kama nyenzo ya uamsho na mabadiliko, linakazia ukweli na kutuelezea kile kilichopungua kwetu na njia ya kufanya, wakati wa uamsho Kuhubiri na kufundisha huwa ni nyenzo muhimu ya wakati wote inayotumika kusema na mioyo yetu, lenyewe linafunua dhambi zetu, linatuonyesha njia na kutupa tumaini na namna ya kumtafuta Mungu na kudumisha uhusiano na yeye, Ezra alipata uamsho, kwa sababu alirudisha moyo wake kwenye mkazo au msingi wa uamsho huo ambao ndio neno la Mungu. Mitume nyakati za kanisa la kwanza walihakikisha kuwa wanabaki katika kulihudumia neno, hii ni kwa sababu walikuwa na ufahamu wa umuhimu wa kutunza uamsho na uwepo wa Mungu kwa kudumu katika neno

Ezra 7: 10 “Kwa maana huyo Ezra alikuwa ameuelekeza moyo wake kuitafuta sheria ya Bwana, na kuitenda, na kufundisha maagizo na hukumu katika Israeli.”

Matendo 6:3-4 “Basi ndugu, chagueni watu saba miongoni mwenu, walioshuhudiwa kuwa wema, wenye kujawa na Roho, na hekima, ili tuwaweke juu ya jambo hili; na sisi tutadumu katika kuomba na kulihudumia lile Neno.”

Utii kwa Roho Mtakatifu:

Roho Mtakatifu pekee ni Bwana wa uamsho, yeye nndiye anayeweza kuichochea mioyo yetu, na kutupa nguvu za kuwa mashahidi wa Mungu, kwa ujumla tunaweza kusema ya kuwa Uamshio ni kazi ya Roho Mtakatifu, kwa hiyo hata kama wanadamu watautaka uamsho na kuvaa majoho ya kutaka kuuuketa kamwe bila Roho Mtakatifu kuhusika hakuwezi kuweko kwa uamsho, Uamsho wa kweli unakuja tu mara anaposhuka Roho Mtakatifu, bila Roho wa Mungu kutenda kazi ya kuvumisha upepo mifupa mikavu isingeliweza kuwa hai

Ezekiel 37:1-14 “Mkono wa Bwana ulikuwa juu yangu, naye akanichukua nje katika roho ya Bwana, akaniweka chini, katikati ya bonde; nalo limejaa mifupa; akanipitisha karibu nayo pande zote; na tazama, palikuwa na mifupa mingi katika ule uwanda! Nayo, tazama, ilikuwa mikavu sana. Akaniambia, Mwanadamu, je! Mifupa hii yaweza kuishi? Nami nikajibu, Ee Bwana MUNGU, wajua wewe. Akaniambia tena, Toa unabii juu ya mifupa hii, uiambie, Enyi mifupa mikavu, lisikieni neno la Bwana. Bwana MUNGU aiambia mifupa hii maneno haya; Tazama, nitatia pumzi ndani yenu, nanyi mtaishi. Nami nitatia mishipa juu yenu, nami nitaleta nyama iwe juu yenu, na kuwafunika ngozi, na kutia pumzi ndani yenu, nanyi mtaishi; nanyi mtajua ya kuwa mimi ndimi Bwana. Basi nikatoa unabii kama nilivyoamriwa; hata nilipokuwa nikitoa unabii, palikuwa na mshindo mkuu; na tazama, tetemeko la nchi, na ile mifupa ikasogeleana, mfupa kwa mfupa mwenziwe. Nikatazama, kumbe! Kulikuwa na mishipa juu yake, nyama ikatokea juu yake, ngozi ikaifunika juu yake; lakini haikuwamo pumzi ndani yake.  Ndipo akaniambia, Tabiri, utabirie upepo, mwanadamu, ukauambie upepo, Bwana MUNGU asema hivi; Njoo, kutoka pande za pepo nne, Ee pumzi, ukawapuzie hawa waliouawa, wapate kuishi. Basi nikatabiri kama alivyoniamuru; pumzi ikawaingia, wakaishi, wakasimama kwa miguu yao, jeshi kubwa mno. Kisha akaniambia, Mwanadamu, mifupa hii ni nyumba yote ya Israeli; tazama, wao husema, Mifupa yetu imekauka, matumaini yetu yametupotea; tumekatiliwa mbali kabisa.Basi tabiri, uwaambie, Bwana MUNGU asema hivi; Tazama, nitafunua makaburi yenu, na kuwapandisha kutoka katika makaburi yenu, enyi watu wangu, nami nitawaingizeni katika nchi ya Israeli.Nanyi mtajua ya kuwa mimi ndimi Bwana, nitakapoyafunua makaburi yenu, na kuwatoa ninyi katika makaburi yenu, enyi watu wangu. Nami nitatia roho yangu ndani yenu, nanyi mtaishi, nami nitawawekeni katika nchi yenu, nanyi mtajua ya kuwa mimi, Bwana, nimesema hayo, na kuyatimiza, asema Bwana.”

Luka 24:49 “Na tazama, nawaletea juu yenu ahadi ya Baba yangu; lakini kaeni humu mjini, hata mvikwe uwezo utokao juu.”

Matendo 1:8 “Lakini mtapokea nguvu, akiisha kuwajilia juu yenu Roho Mtakatifu; nanyi mtakuwa mashahidi wangu katika Yerusalemu, na katika Uyahudi wote, na Samaria, na hata mwisho wa nchi.”

Zekaria 12:10 “Nami nitawamwagia watu wa nyumba ya Daudi, na wenyeji wa Yerusalemu, roho ya neema na kuomba; nao watamtazama yeye ambaye walimchoma; nao watamwombolezea, kama vile mtu amwombolezeavyo mwanawe wa pekee; nao wataona uchungu kwa ajili yake, kama vile mtu aonavyo uchungu kwa ajili ya mzaliwa wake wa kwanza.”

Roho Mtakatifu anaweza kuanza na mtu mmoja au wawili tu na akaweka mzigo wa maombi ndani yao na kupitia wao wengine wakaambukizwa, kumbuka kuwa hatuwezi hata kuomba au kufunga bila msaada wa Mungu, ni kazi ya Mungu Roho Mtakatifu, kuamsha roho zetu, kwa hiyo unaweza kuanza peke yako, usitegemee kuwepo kwa uamsho wa ujumla, tegemea kuanza wewe, Roho Mtakatifu hutoa nguvu ya kuomba, huleta mvuto wa toba, nguvu ya kuhubiri na kuokolewa kwa wengi na Mungu kuwatumia wengi, kwa ujumla tunaweza kusema Roho Mtakatifu ndiye wa Muhimu zaidi kwa kazi ya uamsho: Na bado uamsho ni neema ya Mungu mwenyewe kwa kanisa lake na watu wake,sisi tuna sehemu ndogo sana ya kufanya lakini yeye ndiye mshika dau, na ndiye mwenye kuamsha nia na neema ndani yetu, aamshe nia ndani yetu kuombea viongozi wa kanisa wasichoke, kuombea mikutani ya injili, kuamsha nia ya kusifu na kuabudu, kuamsha ibada zenye nguvu,  kuamsha karama na vipawa vya Roho Mtakatifu, kuamsha nia ya vikundi vya maombi, kuamsha nia ya kusoma neno, kuamsha Imani, kuamsha kiu na hamu na shauku ya kutafuta na kudumisha uhusiano na Mungu, na kuhakikisha kuwa upendo unatawala katika kanisa la Mungu.
 

Na Rev. Innocent Samuel Kamote

Mkuu wa wajenzi mwenye hekima!

0718990796.



Hakuna maoni: