Jumamosi, 13 Julai 2024

Ninyi si wa ulimwengu huu!

 

Yohana 15:18-21 “Iwapo ulimwengu ukiwachukia, mwajua ya kuwa umenichukia mimi kabla ya kuwachukia ninyi. Kama mngekuwa wa ulimwengu, ulimwengu ungewapenda walio wake; lakini kwa kuwa ninyi si wa ulimwengu, bali mimi naliwachagua katika ulimwengu, kwa sababu hiyo ulimwengu huwachukia. Likumbukeni lile neno nililowaambia, Mtumwa si mkubwa kuliko bwana wake. Ikiwa waliniudhi mimi, watawaudhi ninyi; ikiwa walilishika neno langu watalishika na lenu. Lakini haya yote watawatenda kwa ajili ya jina langu, kwa kuwa hawamjui yeye aliyenipeleka.”




Utangulizi:

Iwapo ulimwengu ukiwachukia, mwajua ya kuwa umenichukia mimi kabla ya kuwachukia ninyi. Yesu alikuwa akimaanisha ulimwengu utatuchukia kabisa, kwa sababu kwanza ulimwengu ulimchukia Kristo, Kwa hiyo kila mwanafunzi wa Yesu Kristo hapaswi kuona jambo hilo kuwa ni jambo geni, Kama ulimwengu ulimchukia Kristo kwa vyovyote vile hauwezi kuwakubali wafuasi wake.

Mathayo 10:22-25 “Nanyi mtakuwa mkichukiwa na watu wote kwa ajili ya jina langu; lakini mwenye kuvumilia hata mwisho, ndiye atakayeokoka. Lakini watakapowafukuza katika mji huu, kimbilieni mwingine; kwa maana ni kweli nawaambia, Hamtaimaliza miji ya Israeli, hata ajapo Mwana wa Adamu. Mwanafunzi hampiti mwalimu wake, wala mtumwa hampiti bwana wake.Yamtosha mwanafunzi kuwa kama mwalimu wake, na mtumwa kuwa kama bwana wake. Ikiwa wamemwita mwenye nyumba Beelzebuli, je! Si zaidi wale walio wa nyumbani mwake?

Ulimwengu unachukizwa sana na watu waliomwamini Yesu na kumfuata, kwa sababu sio wa ulimwengu huu, wakati wanafunzi wa Yesu watatambulikwa kwa upendo wao kwa watu, watu wa ulimwengu huu watajulikana kwa chuki na wivu dhidi ya watu wa Mungu, wanafunzi wa Yesu sio wa ulimwengu huu kwa sababu wameitwa kutoka ulimwenguni kuingia katika ufalme wa mwana wa pendo lake, na kuuacha ufalme wa giza, kwa hiyo tuwapo katika maisha haya sisi wenyeji wetu uko mbinguni, na kwa sababu hiyo mkuu wa ulimwengu huu hawezi kuwa na furaha na watu waliookolewa, kwa sababu wao wameuacha ufalme wake, na hivyo anachukizwa nao, wale walio wa ulimwengu huu wao ndio wenyeji wa ufalme wa shetani au ufalme wa giza na hivyo hauwezi kuweko urafiki kati ya nuru na giza, kweli na uongo, na hivyo hakuwezi kuweko kwa Amani na upendo wa kweli kutoka katika dunia hii inayoongozwa na mfumo wa yule muovu, wala watu wa Mungu wasitarajie ya kuwa dunia itawatendea haki, kwa sababu mfumo wa ulimwengu huu unawatema!, Mfumo wa ulimwengu huu uko chini ya Shetani ambaye kimsingi hana nguvu kama za Bwana wetu Yesu, lakini hata hivyo anatawala mfumo wa uasi wa dunia na kunyunyizia ushawishi wake duniani. 

Yohana 14:30-31 “Mimi sitasema nanyi maneno mengi tena, kwa maana yuaja mkuu wa ulimwengu huu, wala hana kitu kwangu. Lakini ulimwengu ujue ya kuwa nampenda Baba; na kama vile Baba alivyoniamuru; ndivyo nifanyavyo. Ondokeni, twendeni zetu.”       

Tutajifunza somo hili ninyi si wa ulimwengu huu kwa kuzingatia vipengele vitatu vifuatavyo:-


·         Ufahamu kuhusu mkuu wa ulimwengu huu.

·         Kuchukiwa kwa watu wasio wa ulimwengu huu.

·         Jinsi watu wasio wa ulimwengu huu wanavyopaswa kuishi.


Ufahamu kuhusu mkuu wa ulimwengu huu.

Ni muhimu kufahamu kuwa Shetani ana majina mengi yanayomtambulisha kama mwenye mamlaka na ulimwengu huu, Katika maandiko Yesu anamtaja kama mkuu wa ulimwengu huu Katika

Yohana 14:30 Mimi sitasema nanyi maneno mengi tena, kwa maana yuaja mkuu wa ulimwengu huu, wala hana kitu kwangu.  

Katika biblia ya kiingereza maneno hayo yanasomeka “I will not speak with you much longer, for the PRINCE OF THIS WORLD is coming. He has no hold on me” kwa hiyo shetani anaitwa mkuu wa ulimwengu huu, au kwa jina lingine, mungu wa dunia hii angalia au mfalme wa dunia hii, Kwa hiyo kimsingi Shetani ni mtawala wa dunia hii.

2Wakorintho 4:3-4 “Lakini ikiwa injili yetu imesitirika, imesitirika kwa hao wanaopotea; ambao ndani yao mungu wa dunia hii amepofusha fikira zao wasioamini, isiwazukie nuru ya injili ya utukufu wake Kristo aliye sura yake Mungu.”  

Unaona katika andiko hili Shetani anaitwa MUNGU WA DUNIA HII.  Aidha katika maandiko mengine Shetani anaitwa MFALME WA UWEZO WA ANGA “The Prince of the air” hili unaweza kuliona katika kitabu cha Waefeso

Waefeso 2:1-3 Nanyi mlikuwa wafu kwa sababu ya makosa na dhambi zenu; ambazo mliziendea zamani kwa kuifuata kawaida ya ulimwengu huu, na kwa kumfuata mfalme wa uwezo wa anga, roho yule atendaye kazi sasa katika wana wa kuasi; ambao zamani, sisi sote nasi tulienenda kati yao, katika tamaa za miili yetu, tulipoyatimiza mapenzi ya mwili na ya nia, tukawa kwa tabia yetu watoto wa hasira kama na hao wengine.”

Hii ina maana gani? Ni muhimu kufahamu kuwa katika lugha ya Kiyunani neno Prince of this world, mkuu wa ulimwengu huu, god of this age, mungu wa dunia hii, ruler of the kingdom of air, mkuu wa uweza wa anga huyu kwa kwa kiyunani anaitwa KOSMOKRATOR  kwa kiingereza COSMOCRATOR  maana yake RULER OF THE WORLD  neno hilo Kosmokrator limetokana na lugha ya asili ya dini za kipagani hususani Wanostiki na Wamarcion wakimaanisha ni lugha ya kiufundi ya kumtambulisha Shetani kutokana na kazi zake za uendeshaji wa ulimwenguni kwa hivyo utaweza kuona jina hilo Kosmokrator ni mkuu wa anga, au mtawala wa dunia hii au mwenye ushawishi wa akili na tabia na mwenendo, malengo, matumaini, falsafa, elimu, biashara, mawazo, fikra, ujasusi, udhibiti, na utaratibu wa kila kitu hapa duniani. Katika ulimwengu wa watu wasiookolewa ni muhimu ikafahamika wazi kuwa ulimwengu uko chini ya huyu Kosmokrator yaani Shetani. Kwa hiyo mifumo yote ya uendeshaji wa dunia hii na ushawishi wake uko chini ya mkuu wa anga anayetenda kazi sasa kwa wana wa kuasi.

Yohana 12:31Sasa hukumu ya ulimwengu huu ipo; sasa mkuu wa ulimwengu huu atatupwa nje”. Kwa hiyo Mkuu wa anga anaitwa Kosmokrator wakati ulimwengu na mfumo wake wote unaitwa Kosmos,  Mapambo  na vipodozi vyote vinaitwa Kosmetikos, yaani art of beautification kwa hiyo neno Kosmos lilitumika pia kuelezea mfumo wa ulimwengu na ndio maana nyakati za kanisa la Kwanza mtu aliyeonyesha kuupenda sana ulimwengu alifikiriwa pia amekuwa adui wa Mungu.

Yakobo 4:4 . “Enyi wazinzi, hamjui ya kwamba kuwa rafiki wa dunia ni kuwa adui wa Mungu? Basi kila atakaye kuwa rafiki wa dunia hujifanya kuwa adui wa Mungu.”

Kwa hiyo Maandiko yanapomtaja shetani kama mkuu wa ulimwengu huu, yanafunua ule ukweli ya kuwa katika ulimwengu huu wako watu wanaoongozwa na mfumo wake na wanaofuata mfumo wake na wako chini ya mfumo huo na pia wale waliomwamini Yesu wako katika mfumo mwingine wanaishi duniani lakini wakiwa wamehamishwa katika ufalme huo wa giza na kuingizwa katika mfumo wa ufalme wa mwana wa pendo lake yaani Pendo la Mungu. Hii ina maana gani ina maana ya kuwa watu waliookoka hawako chini ya utawala wa shetani, kwa hiyo wao sio wa ulimwengu huu

Wakolosai 1:13-14 “Naye alituokoa katika nguvu za giza, akatuhamisha na kutuingiza katika ufalme wa Mwana wa pendo lake; ambaye katika yeye tuna ukombozi, yaani, msamaha wa dhambi;”             

Kuchukiwa kwa watu wasio wa ulimwengu huu

Kwa sababu mtawala wa ulimwengu huu yaani shetani amepokonywa mateka yaani watu waliookolewa, wakahamishwa katika ufalme wa Mungu, Shetani amekuwa adui mkubwa sana wa watu wa Mungu na anachukizwa nao sana. Yesu akilijua hilo anatuwekea wazi, kuwa nasi tutachukiwa sana na ulimwengu na hii ni kwa sababu ulimwengu huo huo haukumkubali Bwana Yesu.

Yohana 15:18-21 “Iwapo ulimwengu ukiwachukia, mwajua ya kuwa umenichukia mimi kabla ya kuwachukia ninyi.Kama mngekuwa wa ulimwengu, ulimwengu ungewapenda walio wake; lakini kwa kuwa ninyi si wa ulimwengu, bali mimi naliwachagua katika ulimwengu, kwa sababu hiyo ulimwengu huwachukia. Likumbukeni lile neno nililowaambia, Mtumwa si mkubwa kuliko bwana wake. Ikiwa waliniudhi mimi, watawaudhi ninyi; ikiwa walilishika neno langu watalishika na lenu. Lakini haya yote watawatenda kwa ajili ya jina langu, kwa kuwa hawamjui yeye aliyenipeleka.”

Yesu anaendelea kukazia kuwa mtumwa si mkubwa kuliko Bwana wake, maana yake hali ile ile ambayo watu wanamfanyia Bwana wako ni hali ile ile ndiyo watakayo mfanyia mtumwa wake, Hali anayofanyiwa mwenye nyumba, ndiyo hiyo hiyo watakayofanyiwa wale wa nyumbani mwake, ikiwa walimsulubisha Bwana wetu Yesu Kristo hali kadhalika wanafunzi wa Yesu Kristo watasulubiwa na kupata mateso mengi, kwa sababu nao wataishi na kufanya kazi kama zile zile alizozifanya Yesu Kristo, Yesu ni Nuru ya ulimwengu hali kadhalika watu wa Mungu ni nuru ulimwenguni, na watu wa dunia hii wanapenda giza na ndio maana walimsulubisha Yesu Kristo wote wapendao kuishi kwa hali itokanayo na Kristo Yesu wataudhiwa

2Timotheo 3:10-12 “Bali wewe umeyafuata mafundisho yangu, na mwenendo wangu, na makusudi yangu, na imani, na uvumilivu,na upendo, na saburi; tena na adha zangu na mateso, mambo yaliyonipata katika Antiokia, katika Ikonio, na katika Listra, kila namna ya adha niliyoistahimili, naye Bwana aliniokoa katika hayo yote.Naam, na wote wapendao kuishi maisha ya utauwa katika Kristo Yesu wataudhiwa.”

Kwa hiyo wapenzi msione kuwa ni ajabu watu waliompokea Yesu, wakikutana na vikwazo vingi, wakikataliwa, wakidharauliwa, wakichukiwa na dunia, wakifanyiwa fitina, wakizushiwa, wakidhulumiwa, wakifanyiwa hila, wakihuzunishwa kwa namna mbalimbali, wakibaniwa, wakisalitiwa, wakitafuta kuuawa, Wakristo watapata mateso na uonevu kwa sababu ya Imani yao, watakutana na vipingamizi kwa sababu ya mifumo ya kipinzani ya dunia hii,  watatengwa na jamii na familia zao na dini zao,  kwa sababu hawakubaliki na mfumo wa ulimwengu huu, mifumo ya Kosmokrator iko kuanzia ngazi ya ulimwengu, mabara, mataifa, mikoa, wilaya na kila kijiji, na katika kila eneo nguvu ya ushawishi wa mkuu wa anga katika eneo hilo atapingana vikali na wakristo wa eneo husika akitumia aina ya ushawishi wake, katika eneo husika kuwapiga vita wakristo na vita hii iko katika ulimwengu wa roho.

Waefeso 6:10-13 “Hatimaye, mzidi kuwa hodari katika Bwana na katika uweza wa nguvu zake. Vaeni silaha zote za Mungu, mpate kuweza kuzipinga hila za Shetani. Kwa maana kushindana kwetu sisi si juu ya damu na nyama; bali ni juu ya falme na mamlaka, juu ya wakuu wa giza hili, juu ya majeshi ya pepo wabaya katika ulimwengu wa roho.Kwa sababu hiyo twaeni silaha zote za Mungu, mpate kuweza kushindana siku ya uovu, na mkiisha kuyatimiza yote, kusimama.”

Katika vita hivi na mfumo wa ulimwengu huu wakristo hawapaswi kuogopa kwa sababu mkuu wa ulimwengu huu hana kitu kwa Yesu Kristo na zaidi ya yote neno la Mungu limetuthibitishia wazi ya kuwa aliye ndani yetu ni mkuu kuliko yeye aliye ulimwenguni.

1Yohana 4:4-6 “Ninyi, watoto wadogo, mwatokana na Mungu nanyi mmewashinda, kwa sababu yeye aliye ndani yenu ni mkuu kuliko yeye aliye katika dunia. Hao ni wa dunia; kwa hiyo wanena ya dunia na dunia huwasikia Sisi twatokana na Mungu. Yeye amjuaye Mungu atusikia; yeye asiyetokana na Mungu hatusikii. Katika hili twamjua Roho wa kweli, na roho ya upotevu.”

Watu wa Mungu wanapaswa kuwa hodari Duniani, wanapaswa kuwa na imani, wanapaswa kuwa wapambanaji, wanapaswa kutumia silaha zote walizopewa kushughulika na wakuu wa anga katika mazingira yetu na kuharibu nguvu ya ushawishi inayotenda kazi kulingana na mazingira yetu na kwa kufanya hivyo tutapata upenyo, aidha kila tunapoendelea kuihubiri injili tunaendelea kumpa shida mkuu wa anga na kumpokonya mateka wake.  

Jinsi watu wasio wa ulimwengu huu wanavyopaswa kuishi

1.       Kuishi kwa kiasi chini ya neema ya Mungu –  kila mtu aliyeokolewa, aliokolewa kwa neema na kwa sababu hiyo hiyo hatuna budi kuendelea kuishi kwa neema, shetani hatataka mtu aliyeokolewa kwa neema aendelee kufurahia neema hiyo na kwa vyovyote vile atatupandikizia falsafa za dunia hii za kututaka tupate kibali kwa Mungu kwa njia ya tendo au matendo fulani, ni muhimu kukumbuka na kufahamu kuwa dini zote za uongo duniani zina mfumo wa kukutaka upate kibali kwa Mungu kwa njia ya matendo, Uislamu unakazia matendo mema, Budha, Hindu, Confucianism, Sikhism,Taoism, Shintoism, Judaism n.k  au kuupata wokovu kwa kazi, au kwa matendo mema, jambo hilo ni kinyume na kweli ya Mungu kwa sababu wokovu, na uzima wa milele ni zawadi kutoka kwa Mungu, ni kipawa ni karama ambayo kamwe haitokani na nafsi zetu wala matendo yetu  bali neema ya Mungu, tunaokolewa kwa neema na tunaendelea kuishi kwa neema tukimpendeza na kusaidiwa na Roho wake Mtakatifu kumpendeza Mungu kwa neema yake.

 

Waefeso 2:8-9 “Kwa maana mmeokolewa kwa neema, kwa njia ya imani; ambayo hiyo haikutokana na nafsi zenu, ni kipawa cha Mungu; wala si kwa matendo, mtu awaye yote asije akajisifu.”

 

2.       Kuishi kwa Imani isiyotikisika -  watu wa Mungu watapitia dhiki na mateso mengi lakini mateso yao au yetu isiwe sababu ya kuyumba wala kuogopa mateso, watakatifu waliotutangulia waliishi kwa Imani isiyotetereka hata wakati wa majaribu Makubwa walichagua kupata mateso pamoja na watu wa Mungu badala ya kujifurahisha kwa anasa huku wakiikana Imani, Badala yake walikaza kumwangalia Mungu kwa matokeo.

 

Waebrania 11:24-27 “Kwa imani Musa alipokuwa mtu mzima, akakataa kuitwa mwana wa binti Farao; akaona ni afadhali kupata mateso pamoja na watu wa Mungu kuliko kujifurahisha katika dhambi kwa kitambo; akihesabu ya kuwa kushutumiwa kwake Kristo ni utajiri mkuu kuliko hazina za Misri; kwa kuwa aliyatazamia hayo malipo. Kwa imani akatoka Misri, asiogope ghadhabu ya mfalme; maana alistahimili kama amwonaye yeye asiyeonekana.”

               

3.       Kuishi kwa uvumilivu na ustahimilivu - Hakuna jambo linauma kama kuteseka ili hali hujakosea kitu, hata hivyo maandiko yanatutaka kutokuogopa na kutokufadhaika na badala yake kuendelea kustahimili tukivumilia mateso na shida huku tukiiga mfano wa wenzetu ambao walidhihakiwa, walipigwa mijeledi, walifungwa kwa minyororo, walitiwa gerezani, walipigwa kwa mawe, walikatwa kwa misumeno lakini kwaajili ya Imani katika Mungu na upendo wao kwa Kristo walikubali hata kuuawa kuliko kumkana Bwana.

 

1Petro 3:14 “Lakini mjapoteswa kwa sababu ya haki mna heri. Msiogope kutisha kwao, wala msifadhaike; bali mtakaseni Kristo Bwana mioyoni mwenu.”

 

Waebrania 11:35-38 “Wanawake walipokea wafu wao waliofufuliwa. Lakini wengine waliumizwa vibaya hata kuuawa, wasikubali ukombozi, ili wapate ufufuo ulio bora; wengine walijaribiwa kwa dhihaka na mapigo, naam, kwa mafungo, na kwa kutiwa gerezani; walipigwa kwa mawe, walikatwa kwa misumeno, walijaribiwa, waliuawa kwa upanga; walizunguka-zunguka wakivaa ngozi za kondoo na ngozi za mbuzi; walikuwa wahitaji, wakiteswa, wakitendwa mabaya; (watu ambao ulimwengu haukustahili kuwa nao), walikuwa wakizunguka-zunguka katika nyika na katika milima na katika mapango na katika mashimo ya nchi.”

 

4.       Kutokuifuta namna ya dunia hii –  Nyakati za kanisa la Kwanza wanafunzi wa Bwana walijitolea kuishi maisha ya uadilifu na kujitofautisha sana na mifumo ya ulimwengu huu, neno namna ya dunia hii maana yake  ni kushi chini ya kiwango, au chini ya uadilifu neno linalotumika hapo standard of this world au Pattern of this world kwa kiyunani suschÄ“matizo yaani Fashion au design au model, au alike  kwa hiyo lazima watu wa Mungu wajitofautishe na watu wa dunia hii katika mtindo wao wa maisha, neno la Mungu linaagiza hivyo na neema ya Mungu itatusaidia kutufundisha namna ya kuishi zaidi ya kiwango cha dunia hii nje ya muundo 

 

Warumi 12:2 “Wala msiifuatishe namna ya dunia hii; bali mgeuzwe kwa kufanywa upya nia zenu, mpate kujua hakika mapenzi ya Mungu yaliyo mema, ya kumpendeza, na ukamilifu.”

 

Tito 11:11-12 “Maana neema ya Mungu iwaokoayo wanadamu wote imefunuliwa; nayo yatufundisha kukataa ubaya na tamaa za kidunia; tupate kuishi kwa kiasi, na haki, na utauwa, katika ulimwengu huu wa sasa;”           

 

5.       Kuonyesha upendo uzidio – Pamoja na changamoto ambazo ulimwengu utatuletea kutokana na mfumo wake watu wa Mungu ambao wao sio wa ulimwengu huu wanapaswa kuendelea kuonyesha upendo mkubwa kwa wengine hususani wale wanaotuchukia na kufikiriwa kuwa ni adui zetu, kuwapenda maadui au kuwaombea wale wanaotuchukia na kuishi kwa kuonyesha upendo uzidio na hii sio hali ya kawaida kwa ulimwengu huu kwa kufanya hivyo tutawavuta wale watu wa ulimwengu huu kuona na kujua ya kuwa kuna kitu cha ziada katika Kristo.

 

Mathayo 5:43-46 “Mmesikia kwamba imenenwa, Umpende jirani yako, na, Umchukie adui yako; lakini mimi nawaambia, Wapendeni adui zenu, waombeeni wanaowaudhi, ili mpate kuwa wana wa Baba yenu aliye mbinguni; maana yeye huwaangazia jua lake waovu na wema, huwanyeshea mvua wenye haki na wasio haki. Maana mkiwapenda wanaowapenda ninyi mwapata thawabu gani? Hata watoza ushuru, je! Nao hawafanyi yayo hayo?

 

Matendo 7:58-60 “wakamtoa nje ya mji, wakampiga kwa mawe. Nao mashahidi wakaweka nguo zao miguuni pa kijana mmoja aliyeitwa Sauli. Wakampiga kwa mawe Stefano, naye akiomba, akisema, Bwana Yesu, pokea roho yangu. Akapiga magoti, akalia kwa sauti kuu, Bwana, usiwahesabie dhambi hii. Akiisha kusema haya akalala. Na Sauli alikuwa akiona vema kwa kuuawa kwake.”

 

6.       Kuvaa silaha zote za Mungu - watu wasio wa ulimwengu huu wako vitani, na hivyo maandiko yanaagiza kuwa wavae silaha zote za Mungu kama inavyoelezwa katika kitabu cha Waefeso

 

Waefeso 6:11-18 “Vaeni silaha zote za Mungu, mpate kuweza kuzipinga hila za Shetani. Kwa maana kushindana kwetu sisi si juu ya damu na nyama; bali ni juu ya falme na mamlaka, juu ya wakuu wa giza hili, juu ya majeshi ya pepo wabaya katika ulimwengu wa roho. Kwa sababu hiyo twaeni silaha zote za Mungu, mpate kuweza kushindana siku ya uovu, na mkiisha kuyatimiza yote, kusimama. Basi simameni, hali mmejifunga kweli viunoni, na kuvaa dirii ya haki kifuani, na kufungiwa miguu utayari tupatao kwa Injili ya amani; zaidi ya yote mkiitwaa ngao ya imani, ambayo kwa hiyo mtaweza kuizima mishale yote yenye moto ya yule mwovu. Tena ipokeeni chapeo ya wokovu, na upanga wa Roho ambao ni neno la Mungu; kwa sala zote na maombi mkisali kila wakati katika Roho, mkikesha kwa jambo hilo na kudumu katika kuwaombea watakatifu wote;”

 

Hiyo inaashiria kuwa tunapaswa kuwa tayari katika hali ya kiroho kukabiliana na utendaji wa mkuu wa anga na nguvu zake za ushawishi na uovu duniani, ili kujilinda katika vita tuliyonayo kiroho, Kila mkristo kwa kuwa anajua ya kuwa yuko katikati ya adui anapaswa kuwa na msimamo thabiti katika Imani na kupambana kwa ujasiri kwa neema ya Mungu kuweza kuzishinda hila zote za adui zinazozuia ukuaji wa ufalme wa Mungu kwa njia ya injili. Wewe mwenyewe pia ukiyalinda maisha yako kwa kuwa uko vitani, uongezewe neema!

Na Rev. Innocent Samuel Kamote

Mkuu wa wajenzi mwenye Hekima!      

Hakuna maoni: