Jumapili, 21 Julai 2024

Utamlilia Sauli hata lini?


1Samuel 16:1-3 “Bwana akamwambia Samweli, Hata lini utamlilia Sauli, ikiwa mimi nimemkataa asiwamiliki Israeli? Ijaze pembe yako mafuta, uende, nami nitakupeleka kwa Yese, Mbethlehemi; maana nimejipatia mfalme katika wanawe. Samweli akasema, Nawezaje kwenda? Sauli akipata habari, ataniua. Basi Bwana akasema, Chukua ndama pamoja nawe, ukaseme, Nimekuja ili kumtolea Bwana dhabihu. Ukamwite Yese aje kwenye dhabihu, nami nitakuonyesha utakayotenda; nawe utamtia mafuta yule nitakayemtaja kwako.”


Utangulizi:

Kaka zangu dada zangu Leo tutachukua muda kiasi kutafakari ujumbe wa Muhimu wenye kichwa “Utamlilia Sauli Hata lini?” Kama tulivyosoma katika kifungu cha msingi, ujumbe huu una maana kubwa na zaidi sana leo unatufundisha umuhimu wa kusahau mambo yaliyopita ambayo kimsingi yanaweza kuwa kikwazo cha kutupeleka katika mambo mapya au hatua nyingine ambayo Mungu ametuandalia. Wote tutakuwa tunakumbuka kuwa Mungu alimfunulia Samuel Nabii kuhusu Mfalme Mpya wa Israel na kumuagiza akampake mafuta.

1Samuel 9:15-17 “Basi Bwana alikuwa amemfunulia Samweli, siku moja kabla Sauli hajamwendea, akisema, Kesho, wakati kama huu, nitakuletea mtu kutoka nchi ya Benyamini, nawe mtie mafuta ili awe mkuu juu ya watu wangu Israeli, naye atawaokoa watu wangu na mikono ya Wafilisti; maana nimewaangalia watu wangu, kwa sababu kilio chao kimenifikilia.Hata Samweli alipomwona Sauli, Bwana akamwambia, Huyu ndiye niliyekuambia habari zake; huyu ndiye atakayewamiliki watu wangu.”                

Pamoja na kuwa ni kweli Sauli alikuwa ni chaguo la Mungu, Na Samuel alimtia mafuta Lakini ulifika wakati ambapo Mungu alikuwa na mpango mwingine, na hivyo alimkataa Sauli na kumtaka nabii Samuel ampake mafuta Mfalme mwingine mwenye nguvu zaidi na mwenye kuupendeza moyo wake na aliye mwema kuliko Sauli, Mfalme huyo alikuwako Bethelehemu katika nyumba ya Yese. Kukataliwa kwa Sauli kuliwekwa wazi mapema kwa neno la kinabii ona;-

1Samuel 15:26-28 “Samweli akasema, Sitarudi pamoja nawe; kwa sababu umelikataa neno la Bwana, Bwana naye amekukataa wewe, usiwe mfalme wa Israeli. Naye Samweli alipogeuka, aende zake, Sauli akaushika upindo wa vazi lake, nalo likararuka. Basi Samweli akamwambia, Leo Bwana amekurarulia ufalme wa Israeli, naye amempa jirani yako, aliye mwema kuliko wewe

Hata hivyo Samuel kama nabii inaonekana aliendelea Kumuombea neema Saul kwa majuma kadhaa, alimpenda, alitamani aendelee kuwa naye, ilikuwa ni tabia ya Samuel kuwaombea wana wa Israel na mfalme pia kwa mujibu wa maandiko Samuel kuacha kuwaombea Israel kwake ilikua ni kama kufanya dhambi

1Samuel 12:23 “Walakini mimi, hasha! Nisimtende Bwana dhambi kwa kuacha kuwaombea ninyi; lakini nitawaelimisha katika njia iliyo njema, na kunyoka

Kwa hiyo huenda Samuel aliendelea kumuombea Sauli kwa Mungu,  na hakuacha alisikitika moyoni kumpoteza kijana yule mzuri aliyemtia mafuta yeye mwenyewe shujaa, mtu mrefu Mzuri kutoka kabila la Benjamin lakini Mungu aliyakataa maombi ya Samuel kwa sababu alikuwa amekusudia kuwapa Israel Shujaa, kijana mzuri zaidi, anayeupendeza Moyo wa Mungu mtu aliye mwema na atakayekuwa bara kubwa kwa Israel, Hivyo Mungu alimkemea Samuel na kumuuliza utaendelea kumlilia Sauli mpaka lini ikiwa mimi nimemkataa, inawezekana ikawa ni stori nzuri sana na imenyooka haiitaji tafasiri yoyote, lakini leo hii katika kisa hiki, Mungu anataka kusema nasi kuhusu swala la kuachilia Mambo ya kale  ili aweze kutuingiza katika mambo mapya, hupaswi kukaa chini na kuyalilia mambo yaliyopia hata kama ni mazuri kiasi gani kwani kuyalilia hayo kunatufanya tusipige hatua katika kuuendea ukurasa mpya ambao Mungu anataka uufungue, ili tukue na kuelekea katika kiwango kingine, Tutajifuza somo hili Utamlilia Sauli Hata lini kwa kuzingatia vipengele vitatu vifuatavyo:-


·         Umuhimu wa kusahau yaliyopia.

·         Umuhimu wa kutambua mapenzi ya Mungu.

·         Utamlilia Sauli hata lini?.


Umuhimu wa kusahau yaliyopita.

1Samuel 16:1 “Bwana akamwambia Samweli, Hata lini utamlilia Sauli, ikiwa mimi nimemkataa asiwamiliki Israeli? Ijaze pembe yako mafuta, uende, nami nitakupeleka kwa Yese, Mbethlehemi; maana nimejipatia mfalme katika wanawe.”

Ni muhimu kufahamu kuwa Mungu anapokuwa na mpango mpya katika maisha yetu, anapenda tuelewe na kusonga mbele na kuyasahau yaliyopita, siku zote kuendelea kulia lia kwaajili ya mambo ya zamani kunaweza kutuzuia kuona yale mapya ambayo Mungu ametuwekea mbele yetu, na siku zote mbele ni kuzuri zaidi, kwa hiyo ni lazima tuukubali kusahau yaliyopita, ni vigumu sana wakati mwingine kusahau yaliyo nyuma na wakati mwingine inaonekana kama ni jambo lisilowezekana lakini historia ya nyuma inaweza kuwa kikwazo kikubwa cha mpango na mapenzi ya Mungu kwaajili yetu na kwa sababu hiyo ni lazima tuyachuchumilie yaliyo mbele na kukubali kusahau yote yaliyopita.

Wafilipi 3:13-14 “Ndugu, sijidhanii nafsi yangu kwamba nimekwisha kushika; ila natenda neno moja tu; nikiyasahau yaliyo nyuma, nikiyachuchumilia yaliyo mbele; nakaza mwendo, niifikilie mede ya thawabu ya mwito mkuu wa Mungu katika Kristo Yesu.”

Paulo mtume aliyepitia dhiki na mateso mengi sana Hakubali hata kidogo kukaa katika hayo lakini wakati wote alikuwa akijitahidi kuwaza mbele, Ni mapenzi ya Mungu kwetu kusahau mambo yaliyopita hususani yale ambayo yametuletea maumivu makubwa katika maisha yetu,  au makosa amkubwa ambayo tumewahi kuyafanya huko nyuma, Mungu mwenye rehema na neema wakati wote hutupa nafasi ya pili, na ya tatu na ya nne na ya tano na ya sita na ya saba na ya nane na kadhalika yeye anatutaka wakati wote tusilie kwaajili ya yaliyopita na badaa yake tusonge mbele bila kujali kile ulichokipitia, iweni talaka, au uonevu, au umepoteza kazi, au umeingia katika changamoto zozote nzito, au umekosea sana, au umefiwa au ulifeli vyovyote vile Mungu anatutaka tusonge mbele na kuacha kumlilia Sauli kwa sababu ana mpango mpya nawe, Mwana riadha wakati wote anapaswa kuangalia mbele, na kuendelea na mbio, kwani kuangalia nyuma kunaweza kuwa kikwazo, kwa msingi huo usipoteze muda na maswala yaliyopita yawe mazuri au mabaya wewe angalia mbele, Mungu anayekuwazia mema na mpango mpya!

Isaya 43:18-19 “Msiyakumbuke mambo ya kwanza, wala msiyatafakari mambo ya zamani. Tazama, nitatenda neno jipya; sasa litachipuka; je! Hamtalijua sasa? Nitafanya njia hata jangwani, na mito ya maji nyikani.”

Ilikuwa ngumu kwa Samuel kuacha kumlilia Sauli, kwa kuwa alikuwa Mfalme Mzuri na alipewa na Mungu, Lakini sasa Mungu ana mpango mpya ulio bora zaidi, kwa hiyo, yuko Daudi mwana wa Yese kwaajili yako hivyo sahahu utawala na ufalme uliopita chukua chupa yako umtie mafuta yule ambaye Mungu atakuelekeza     

Umuhimu wa kutambua mapenzi ya Mungu

Mungu alikuwa na mpango mpya kwaajili ya Israel Kama alivyo na mpango mpya kwaajili yako, Mungu alikuwa amechagua mmoja wa wana wa Yese na alikuwa yuko tayari kumpaka mafuta Ili atawale baada ya Sauli na ulikuwa ni wajibu wa Samuel kwenda Bethelemu na Chupa yake ya mafuta  na kumtia mafuta yule ambaye Mungu alikuwa amemkusudia, hapa ulikuweko mtihani wa kuyajua mapenzi ya Mungu na ulikuwepo mpango unaohitaji subira, wakati huo ni lazima tuaachane na mambo tuliyoyazoea kwa sababu Mungu ana mpango mpya, sauti zinaweza kuwa nyingi sana wakati tunauendea mpango mpya wa Mungu na tunaweza kufikiri kuwa ni huu au ule  lakini hatimaye Mungu atakufunulia mpango wake kamili ambao huo Yesu yumo ndani yake, The best is yet to come !

1Samuel 16:6-11 “Ikawa walipokuja, alimtazama Eliabu, akasema, Yakini masihi wa BWANA yupo hapa mbele zake. Lakini Bwana akamwambia Samweli, Usimtazame uso wake, wala urefu wa kimo chake; kwa maana mimi nimemkataa. Bwana haangalii kama binadamu aangaliavyo; maana wanadamu huitazama sura ya nje, bali Bwana huutazama moyo. Ndipo Yese akamwita Abinadabu, akampitisha mbele ya Samweli. Naye akasema, Bwana hakumchagua huyu. Ndipo Yese akampitisha Shama. Naye akasema, wala Bwana hakumchagua huyu. Yese akawapitisha wanawe saba mbele ya Samweli. Samweli akamwambia Yese, Bwana hakuwachagua hawa. Kisha Samweli akamwambia Yese, Watoto wako wote wapo hapa? Naye akasema, Amesalia mdogo wao, na tazama, anawachunga kondoo. Basi Samweli akamwambia Yese, Tuma watu, wamlete; kwa sababu hatutaketi hata atakapokuja huku.”            

Kujua mapenzi ya Mungu kwaajili ya mpango mpya sio kazi nyepesi, ilimsumbua Samuel ilimsumbua Yese, hawakujua mfalme mpya ni nani, na kwakuwa hakuwepo pale walihitaji subira, tunahitaji subira kuyajua mapenzi ya Mungu, Katika maisha yetu tunaweza kukutana na changamoto kama hizi, wakati huu tunapaswa kuongeza uwezo wa kuisikia sauti ya Mungu, na kuwa na moyo wa Subira, ili kuachana na mazoea na kuyajua mapenzi yake kwa hiyo kuna umuhimu wa kuyatambua mapenzi ya Mungu, kuna mambo matatu tu tunaweza kuyafanya wakati huu

1.       Kujaza pembe Mafuta – hii inahusiana na kufanya maandalizi ya kiroho kwa hiyo ni muhimu kwetu kujitoa kwa Roho Mtakatifu, kwa kuomba na kujitakasa na kutubu, tendo hili litatuweka karibu na Roho Mtakatifu  na kutusaidia kuijua sauti yake  na zaidi ya yote inatusaidia kuyatii mapenzi yake na kuyajua

 

1Samuel 16:4-5  “.Samweli akafanya hayo aliyosema Bwana, akaenda Bethlehemu. Wakaja wazee wa mji kumlaki, wakitetemeka, nao wakasema, Je! Umekuja kwa amani? Naye akasema, Naam, kwa amani; nimekuja kumtolea Bwana dhabihu; jitakaseni; njoni pamoja nami kwenye dhabihu. Akawatakasa Yese na wanawe, akawaita kwenye dhabihu

 

Matendo 13:1-3 “Na huko Antiokia katika kanisa lililokuwako palikuwa na manabii na waalimu, nao ni Barnaba, na Simeoni aitwaye Nigeri, na Lukio Mkirene, na Manaeni aliyekuwa ndugu wa kunyonya wa mfalme Herode, na Sauli. Basi hawa walipokuwa wakimfanyia Bwana ibada na kufunga, Roho Mtakatifu akasema, Nitengeeni Barnaba na Sauli kwa kazi ile niliyowaitia. Ndipo wakiisha kufunga na kuomba, wakaweka mikono yao juu yao, wakawaacha waende zao.”

 

2.       Kutii maagizo ya Mungu – Samuel alitii maagizo ya Mungu na kukubalia kumsahau Sauli na akaenda kwa Yese ili kumtia mafuta Daudi, Tunapaswa kuyatii maagizo ya Mungu na kusonga mbele bila kuchelewa, ni muhimu kufahamu kuwa mambo ya zamani yanakamata sana na yanataka kuturudisha nyuma, Lakini Mungu ameruhusu tusonge mbele kwa hiyo hatuna budi kwenda pale Mungu anaposema twende Samuel akafanya hayo aliyoyasema Bwana, akaenda Bethelehemu kule Bwana atakakosema wende nenda na yale maagizo ambayo Bwana amekuagiza kuyafanya yafanye kwa kutumia Hekima chini ya neema yake.

 

3.       Ruhusu Mpango mpya wa Mungu -  Samuel na Yese walikubali mapenzi ya Mungu, alipokuja yeye aliyesubiriwa na asiyetazamiwa Samuel alimtia mafuta kwani Bwana alisema naye huyu ndiye, kwa hiyo walilazimika kumsahau Sauli na kumkubali Daudi, Mambo ya zamani ambayo hayana nafasi tena katika maisha yetu na ambayo hayako katiika mpango wa Mungu ni lazima tuyafukuzilie mbali, ili lile jipya ambalo Mungu amekusudia kulifanya liweze kuchukua nafasi.

 

1Samuel 16:12-13 “Basi akatuma mtu, naye akamleta kwao. Naye alikuwa mwekundu, mwenye macho mazuri, na umbo lake lilikuwa la kupendeza. Bwana akasema, Ondoka, umtie mafuta; maana huyu ndiye. Ndipo Samweli akaitwaa pembe yenye mafuta, akamtia mafuta kati ya ndugu zake; na roho ya Bwana ikamjilia Daudi kwa nguvu tangu siku ile. Basi Samweli akaondoka, akaenda zake Rama.”                

Utamlilia Sauli hata lini?

Utamlilia Sauli hata lini? Ni swali ambalo Mungu alimuuliza Samuel na ni swali ambalo linatuita katika kutafakari maisha yetu, Je kuna jambo bado unalishikilia? bado una shikilia mambo ya zamani ambayo Mungu anataka tuyaache na kuyasahau? Je unajiandaa kwa mambo mapya?  Tunapotulia katika maombi hatuna budi kuendelea kumuomba Mungu atuongoze na kutuandaa na kutuweka tayari ili tukubali kuyatii mapenzi yake, na kupokea kile kipya ambacho Mungu amekikusudia katika maisha yetu  na Mungu ni mwema atakutendea mema usilie!

Kuacha mambo ya zamani kunahitaji ujasiri, na Imani, Samuel alihitaji ujasiri na kukubali mabadiliko kwa Imani, kwa sababu Mungu alimthibitishia kuwa ana mpango bora zaidi kwaajili ya Israel Mpango wenye manufaa sio kwaajili ya Israel tu  bali kwa ulimwengu mzima, Mungu alikuwa amemkusudia mwana wa Daudi kuja kukaa katika kiti cha Enzi milele na huyo ni Yesu Kristo, uwepo wa Mungu uko mbele, Mungu alikuwa amekwisha kumuacha Sauli na sasa Roho Mbaya ilikuwa inamkalia, Mahali ambapo uwepo wa Mungu umeondoka, Shetani na mapepo huchukua nafsi

1Samuel 16:14-15. “Basi, roho ya Bwana ilikuwa imemwacha Sauli, na roho mbaya kutoka kwa Bwana ikamsumbua. Nao watumishi wa Sauli wakamwambia, Angalia, sasa roho mbaya kutoka kwa Mungu inakusumbua.”

Mungu alikwisha ondoa uwepo wake kwa Sauli na kuruhusu mashetani kumkalia, Mungu anapotushauri jambo ni vema kwenda nalo, kwa kuwa huko ndiko uwepo wake unakokwenda hatupaswi kujivunia Sauli tena kwani sasa ni nyumba ya mapepo na uwepo wa Mungu umehama, uwepo wa Mungu sasa ulikuwa uko juu ya Daudi kwa nguvu!

1Samuel 16:13 “Ndipo Samweli akaitwaa pembe yenye mafuta, akamtia mafuta kati ya ndugu zake; na roho ya Bwana ikamjilia Daudi kwa nguvu tangu siku ile. Basi Samweli akaondoka, akaenda zake Rama.”

Acha kulilia ya nyuma Songa mbele Mungu anampango mwema zaidi msahau Sauli, Mungu anaye Daudi wako je utaendelea kumlilia Sauli hata lini ikiwa mimi nimemkataa? Uwepo wa Mungu uko mbele!, Usilie kwaajili ya kazi uliyofukuzwa, usilie kwaajili ya nyumba uliyohama, usilie kwaajili ya mchumba ambaye ameondoka, usilie kwaajili ya mke aliyekuacha, usilie kwaajili ya mume aliyekuacha, usilie kwaajili ya bosi aliyekuacha Mungu anao mpango mwingine kwaajili yako, usilie kwaajili ya uhamisho uliohamishiwa kuna kusudi kubwa na jipya kwaajili ya Mungu. Na Kwaajili yako na familia yako na watu wako!

1Wafalme 9:5 “ndipo nitakapokifanya imara kiti cha ufalme wako juu ya Israeli milele; kama nilivyomwahidia Daudi, baba yako, nikisema, Hutakosa kuwa na mtu wa kukaa katika kiti cha enzi cha Israeli.”

Na Rev. Innocent Samuel Kamote

Mkuu wa wajenzi mwenye Hekima!.

Hakuna maoni: