Ijumaa, 28 Machi 2025

Sisi tunaogopa kuvunja agano!


Daniel 9:3-4 “Nikamwelekezea Bwana Mungu uso wangu, ili kutaka kwa maombi, na dua, pamoja na kufunga, na kuvaa nguo za magunia na majivu. Nikamwomba Bwana, Mungu wangu, nikaungama, nikasema, Ee Bwana, Mungu mkuu, mwenye kutisha, ashikaye maagano na rehema kwao wampendao, na kuzishika amri zake;”


      Rev. Innocent Samuel Kamote akiwa na vijana wa Kimasai Loiborsoit, Simanjiro, Mkoani Manyara


Utangulizi:

Ni Tarehe 15/03/2025 Mida ya Mchana nikiwa kijiji cha Loiborsoit A, Wilayani Simanjiro, Mkoani Manyara, tunaelekea kwenye Harusi ya kimila ya kijana wa rafiki yetu, katika jamii ya kimasai, njiani ninaongozana na kijana wa kimasai Morani (Nyangulo).  Na kijana wa zamani (Kuriyanga) namuuliza harusi hii ya kimila itafungwa saa ngapi ananiambia itafungwa saa nne za usiku, namuuliza ni kwanini haikufungwa kanisani? Kijana wa kimaasai akaniambia, Kanisani? Hapana sisi tunaogopa kuvunja maagano, Hatuwezi kwenda kufunga ndoa ya kanisani kwa sababu tutaapishwa, tutamuahidi Mungu kuwa nitakuwa na mwanamke huyu tu na wengine wote nitawaepuka, na sitawatamani wengine, jambo ambalo ni la uongo na linaweza kuleta laana kwetu, au mwanamke anaweza kunisumbua nikabadili mawazo, kwa nini nimdanganye Mungu na kuapa au kujifunga katika agano ambalo ukweli sitaweza kulitimiza kwa hiyo nafikiri ndoa hii ya kimila isiyo na kiapo chochote ni nzuri na nafuu kuliko zile ndoa zenu za kanisani!

Hili lilinipa kutafakari sana na kunipa swali kubwa la kujiuliza Je wakristo wa leo kweli wanashika maagano? Kwanini ndoa nyingi sana leo zinavunjika tena ndoa za kilokole je wanajua gharama za kuvunja maagano? Je wanahofu na wanajua kuwa Mungu hushika maagano? Je wanajua kuwa kuvunja agano huleta laana na madhara makubwa sana? Je hivi wanajua kuwa ndoa ni agano? Leo hii ndoa nyingi sana zinavunjika hususani za watu wanaojulikana kama waliokoka. Hakimu mmoja alisema siku hizi watu wakija mahakamani wakiwa na madai kuwa wanataka kuachana tunauliza tu ninyi ni wakristo? Wanajibu ndio swali la pili ni wa madhehebu gani? Wakitujibu kuwa ni ya Kipentekoste basi haraka sana tunaandika talaka kwa sababu wao ndio ambao kesi zao tumezichoka na ndio wanaoongoza kwa kuvunja ndoa!  Na ndio wanaoongoza leo kwa kubadili mwelekeo na kuvunja ndoa, kwa hiyo hatuzicheleweshi alisema hakimu huyo! Kwa kweli watu waliookoka hawaogopi kuvunja maagano wala hawajui hatari yake na kama wanajua basi hawajajua madhara makubwa ya kuvunja maagano! Kwa sababu hiyo leo tuarudi tena katika maandiko kujifunza tena kwa kina na mapana na marefu kuhusiana na agano la ndoa na tutaliangalia somo hili kwa kuzingatia vipengele vinne vifuatavyo:-


·         Tofauti ya Agano na maswala mengine.

·         Madhara ya kuvunja agano.

·         Mifano ya watu waliovunja agano na kupata madhara.

·         Mambo ya kufanya unapokuwa umevunja agano.


Tofauti ya Agano na mambo mengine.

Kabla hatujafanya Uchambuzi wa kina kuhusu maana ya neno Agano ni muhimu kwetu tukayachambua mambo mengine muhimu yanayofanana na agano ambayo yatatusaidia kulielewa vema neno Agano ambalo ni la muhimu Zaidi katika ujumbe wetu huu wa leo!

1.      Agano ni tofauti na “Mkataba”. A  contract.

 

Mkataba ni mapatano ya kimaneno au kimaandishi yanayohusisha pande mbili katika kufikia jambo fulani Bila kumuhusisha Mungu; Mkataba unaweza kuwa mkataba wa mauzo, kazi, ajira na kadhalika Kwa kawaida Mtu anapovunja mkataba yule atakayeuvunja kabla ya wakati huwajibika kulipa fidia.

2.      Agano ni tofauti na ”Nadhiri”. A ”Vow” or ” an Oath

 

Tofauti na mkataba Nadhiri ni ahadi anayoitoa mtu akijifunga kwa Mungu huku akitarajia Mungu amfanyie yeye kitu ili yeye atimize kile alichoahidi Mfano

Waamuzi 11:29-31. ”Ndipo roho ya Bwana ikamjilia juu yake Yeftha, naye akapita katika Gileadi na Manase, akapita na katika Mispa ya Gileadi, na kutoka hapo Mispa ya Gileadi akapita kuwaendea wana wa Amoni. Naye Yeftha akamwekea Bwana nadhiri, akasema, Kwamba wewe utawatia wana wa Amoni mkononi mwangu kweli, ndipo itakuwa ya kwamba, kile kitakachotoka katika milango ya nyumba yangu kunilaki, hapo nitakaporudi na amani kutoka kwa hao wana wa Amoni, kitu hicho kitakuwa ni cha Bwana, nami nitakisongeza kiwe sadaka ya kuteketezwa.”   

1Samuel 1:10-11Naye huyo mwanamke alikuwa na uchungu rohoni mwake, akamwomba Bwana akalia sana. Akaweka nadhiri, akasema, Ee Bwana wa majeshi, ikiwa wewe utaliangalia teso la mjakazi wako, na kunikumbuka, wala usinisahau mimi mjakazi wako, na kunipa mimi mjakazi wako mtoto mume, ndipo mimi nitakapompa Bwana huyo mtoto siku zote za maisha yake, wala wembe hautamfikilia kichwani kamwe. Ikawa, hapo alipodumu kuomba mbele za Bwana, Eli akamwangalia kinywa chake.”

Hata hivyo maandiko yanashauri kutokuweka nadhiri na kama mtu ataweka nadhiri anashauriwa kukumbuka kuiondoa, kutokuitendea kazi nadhiri kunaweza kushababisha madhara makubwa kwani Mungu anakumbuka lakini wanadamu tunasahau, kuweka nadhiri na kushindwa kuiondoa ni Upumbavu kwa mujibu wa maandiko ona:-

Muhubiri 5:4-6  Wewe ukimwekea Mungu nadhiri, usikawie kuiondoa; kwa kuwa yeye hawi radhi na wapumbavu; basi, uiondoe hiyo uliyoiweka nadhiri. Ni afadhali usiweke nadhiri, Kuliko kuiweka usiiondoe. Usikiache kinywa chako kuukosesha mwili wako; wala usiseme mbele ya huyo malaika ya kwamba umepitiliwa; kwani Mungu akukasirikie sauti yako, na kuiharibu kazi ya mikono yako?        

Kwa mujibu wa andiko hili, ukiweka nadhiri kisha ukakawia kuiondoa maana yake unafanya upumbavu, kwa hiyo tunashauriwa kuiondoa, na tunaelezwa kuwa ni afahdali kutokuweka nadhiri, kuliko kuiweka usiiondoe kwa kufanya hivyo kinywa chako kinahatarisha maisha yako, na malaika ndio huwa wanakuwa ni mashahidi na wanaofuatilia nadhiri, kutokuondoa nadhiri husababisha Mungu akukasirikie na sio hivyo tu analaani kazi za mikono yako, kwa hiyo ndio kusema kuwa madhara mengine yanatokana na vinywa vyetu wenyewe kwa kuahidi tusiyoweza kuyatekeleza kwa Mungu.

3.      Agano ni tofauti na ”kiapo an Oath

 

Hii ni ahadi anayojiapiza mtu kwa Mungu au kwa mwenzake ili kuuthibitisha ukweli au uaminifu kuwa atafanya yale aliyoahidi au anayoahidi kuyafanya kama kukabidhiwa madaraka, kwa kawaida kutokutimiza kiapo ni dhambi na inaruhusu hukumu ya Mungu, wanadamu ni waongo na ni wachache tu wanaoweza kusimamia yale wanayoyaahidi, Yesu alitahadharisha sana kuhusu swala la kiapo akitutaka wanafunzi wake kuwa tusiape kabisa bali aliagiza kuwa majibu yetu yawe ndio, ndio au Siyo, siyo.

Mathayo 5:33-37  Tena mmesikia watu wa kale walivyoambiwa, Usiape uongo, ila mtimizie Bwana nyapo zako; lakini mimi nawaambia, Usiape kabisa; hata kwa mbingu, kwa maana ndicho kiti cha enzi cha Mungu; wala kwa nchi, kwa maana ndiyo pa kuwekea miguu yake; wala kwa Yerusalemu, kwa maana ndio mji wa Mfalme mkuu. Wala usiape kwa kichwa chako, maana huwezi kufanya unywele mmoja kuwa mweupe au mweusi. Bali maneno yenu yawe Ndiyo, ndiyo; Siyo, siyo; kwa kuwa yazidiyo hayo yatoka kwa yule mwovu.”         

Kwa nini Yesu aliagiza tusiape? Kwa kuwa  inagharimu hukumu  mtu asipotimiza  kiapo, Mungu ni wa kuheshimiwa sana mbingu ni kiti chake cha enzi, inchi ni sehemu yake ya kuwekea miguu yake na Yerusalem ni mji wa mfalme mkuu (masihi) wala kwa kichwa chako kwa sababu huwezo kuongeza au kupunguza siku zako kwa msingi huo basi Yesu alituonya kuhusu kiapo na kututaka kuwa wakweli.

Yakobo 5:12 Lakini zaidi ya yote, ndugu zangu, msiape, wala kwa mbingu wala kwa nchi; wala kwa kiapo kinginecho chote; bali ndiyo yenu na iwe ndiyo, na siyo yenu iwe siyo, msije mkaangukia hukumu.”.

Kuapia/kiapo ndiko kulikopelekea kifo cha Yohana mbatizaji kutokea Mathayo 14:6-10 ”Hata ilipofika sikukuu ya kuzaliwa kwake Herode, binti Herodia alicheza mbele ya watu, akampendeza Herode. Hata akaahidi kwa kiapo ya kwamba atampa lo lote atakaloliomba.Naye, huku akichochewa na mamaye, akasema, Nipe hapa katika kombe kichwa cha Yohana Mbatizaji. Naye mfalme akasikitika; lakini kwa ajili ya viapo vyake, na kwa ajili ya wale walioketi chakulani pamoja naye, akaamuru apewe; akatuma mtu, akamkata kichwa Yohana mle gerezani.

Mungu pia huweza kuapa kwake binafsi kwani hana mkubwa dhidi yake hivyo huweza kujiapia yeye Mwenyewe hii ni ili athibitishe kwetu jinsi alivyo muaminifu

Waebrania 6:13-18 ”Maana wanadamu huapa kwa yeye aliye mkuu kuliko wao; na kwao ukomo wa mashindano yote ya maneno ni kiapo, kwa kuyathibitisha. Katika neno hilo Mungu, akitaka kuwaonyesha zaidi sana warithio ile ahadi, jinsi mashauri yake yasivyoweza kubadilika, alitia kiapo katikati; ili kwa vitu viwili visivyoweza kubadilika, ambavyo katika hivyo Mungu hawezi kusema uongo, tupate faraja iliyo imara, sisi tuliokimbilia kuyashika matumaini yale yawekwayo mbele yetu;” 

Sasa basi Mungu anapoapa kumuelekea mwanadamu kiapo hicho huitwa Agano pia. Na mwanadamu na mwanadamu wanapoapiana mbele za Mungu au Mungu akiwa ni shahidi yao au huku wakimuhusisha Mungu hilo huwa ni AGANO kama ilivyo kwa wanandoa wanapooana kanisani na ikafanyika ibada ya kuwaunganisha kihalali basi hilo huitwa agano. ”Covenant” na likivunjwa lina madhara makubwa kwa pande zote mbili na hususani yule aliyeanza kuvunja agano.

4.      Agano ni nini hasa

Neno agano ambalo kwa kiingereza linajulikana kama Covenant katika lugha ya asili ya kiibrania linajulikana kama ”Berit” ambalo maana yake ni makubaliano yanayofanyika baina ya pande mbili huku Mungu akiwa ni shahidi, Neno Berit pia humaanisha fungamano la kudumu ambalo halikatiki, na linakatika kwa mtu mmoja kufa ili mwenzake awe huru kwa hiyo kwa kiibrania neno Berit pia lilimaanisha ”to Cut” yaani kukata au kukatika au kupasuliwa vipande viwili, kuchinjwa kwa hiyo zamani watu walipofanya agano walichinja mnyama na damu ya mnyama huyo ilimwagika, kisha mnyama alipasuliwa vipande viwili na wahusika walipaswa kupita katikati ya mnyama huyo ili kwamba endapo upande mmoja usipotimiza agano hilo utapata adhabu ya kifo sawa na kifo cha mnyama yule

Mwanzo 15:9-21 ”Akamwambia, Unipatie ndama wa miaka mitatu, na mbuzi mke wa miaka mitatu, na kondoo mume wa miaka mitatu, na hua, na mwana njiwa. Akampatia hao wote, akawapasua vipande viwili, akaweka kila kipande kuelekea mwenzake, ila ndege hakuwapasua. Hata tai walipotua juu ya mizoga Abramu akawafukuza. Na jua lilipokuwa likichwa usingizi mzito ulimshika Abramu, hofu ya giza kuu ikamwangukia. BWANA akamwambia Abramu, Ujue hakika ya kwamba uzao wako utakuwa mgeni katika nchi isiyo yake, watawatumikia watu wale, nao watateswa muda wa miaka mia nne. Hata na taifa lile, watakaowatumikia, nitawahukumu; baadaye watatoka na mali mengi. Lakini wewe utakwenda kwa baba zako kwa amani, utazikwa katika uzee mwema. Na kizazi cha nne kitarudi hapa, maana haujatimia uovu wa Waamori bado. Ikawa, jua lilipokuchwa likawa giza, tazama, tanuru ya moshi na mwenge unaowaka ulipita kati ya vile vipande vya nyama. Siku ile BWANA akafanya agano na Abramu, akasema, Uzao wako nimewapa nchi hii, kutoka mto wa Misri mpaka huo mto mkubwa, mto Frati, Mkeni, na Mkenizi, na Mkadmoni, na Mhiti, na Mperizi, na Mrefai, na Mwamori, na Mkanaani, na Mgirgashi, na Myebusi.”

Katika maandiko hayo tunaona Mungu akifanya agano na Abrahamu, agano la kumpa nchi ya Kanaani, hata hivyo ni Mungu ndiye aliyepita katikati ya mnyama aliyeuawa na sio Abrahamu, hii ilimaanisha kuwa Mungu alikuwa tayari hata kuyatoa maisha yake endapo hangemtimizia Abrahamu ahadi yake hili lilikuwa ni agano, kama agano likivunjwa mtu mmoja aliyevunja agano hilo anatakiwa kufa. Agano linapokuwa limefanyika hata kama upande mmoja utakuwa ulifanya hila na ulikuwa hujazigundua hila hizo, ukamuapia utapaswa kutimiza agano hilo na kama na kama utafanya vinginevyo madhara makubwa sana yatakupata katika maisha yako hususani kifo na laana nyinginezo!

Yoshua 9:1-27 ”Kisha ikawa hapo wafalme wote waliokaa ng'ambo ya pili ya Yordani, hapo penye nchi ya vilima, na katika Shefela, na katika upande wa pwani yote ya bahari kubwa kuikabili Lebanoni, yaani, huyo Mhiti, na Mwamori, na Mkanaani, na Mperizi, na Mhivi, na Myebusi, waliposikia habari ya mambo hayo; ndipo walipojikutanisha pamoja wenyewe kwa wenyewe, ili kupigana na Yoshua, na hao Israeli, kwa nia moja. Lakini wenyeji wa Gibeoni waliposikia habari ya hayo yote Yoshua aliyokuwa amewatenda watu wa Yeriko, na wa Ai,  wao wakatenda kwa hila, nao wakaenda na kujifanya kama ndio wajumbe, wakaenda na magunia makuukuu juu ya punda zao, na viriba vya mvinyo vilivyokuwa vikuukuu vilivyoraruka-raruka, na kutiwa viraka; na viatu vilivyotoboka na kushonwa-shonwa katika miguu yao, na mavao makuukuu waliyokuwa wanavaa; tena mkate wote wa chakula chao ulikuwa umekauka na kuingia koga. Nao wakamwendea Yoshua hata maragoni huko Gilgali, nao wakamwambia yeye na watu wa Israeli, Sisi tumetoka nchi ya mbali sana; basi kwa hiyo fanyeni agano pamoja nasi. Basi watu wa Israeli wakawaambia hao Wahivi, Labda mwakaa kati yetu; nasi tutawezaje kufanya agano nanyi?  Nao wakamwambia Yoshua, Sisi tu watumishi wako. Yoshua akawauliza, Ninyi ni nani? Nanyi mwatoka wapi? Nao wakamwambia, Sisi watumishi wako twatoka nchi iliyo mbali sana, kwa sababu ya jina la Bwana, Mungu wako; kwa kuwa sisi tumesikia sifa zake, na habari ya hayo yote aliyofanya huko Misri, na habari ya hayo yote aliyowatenda wale wafalme wawili wa Waamori, waliokuwa huko ng'ambo ya pili ya Yordani, maana huyo Sihoni, mfalme wa Heshboni, na Ogu, mfalme wa Bashani, aliyekuwa huko Ashtarothi. Kisha wazee wetu, na wenyeji wote wa nchi yetu, walinena nasi na kutuambia, Chukueni vyakula mkononi mwenu kwa ajili ya safari, mwende mkawalaki watu hao, na kuwaambia, Sisi tu watumishi wenu; basi sasa fanyeni agano nasi. Huu mkate wetu tuliutwaa ukali moto katika nyumba zetu, siku hiyo tuliyotoka kuja kwenu, uwe chakula chetu; lakini sasa, tazama, umekauka, na kuingia koga; na viriba vyetu hivi, tulivyovitia divai, vilikuwa ni vipya; sasa, tazama, vimeraruka-raruka; na haya mavazi yetu na viatu vyetu vimekuwa vikuukuu kwa vile tulivyokuja safari ya mbali sana. Basi hao watu wakatwaa katika vyakula vyao, wala wasitake shauri kinywani mwa Bwana. Naye Yoshua akafanya amani pamoja nao, na kufanya agano nao, ili kwamba waachwe hai; na wakuu wa mkutano wakawaapia. Kisha ikawa, mwisho wa siku ya tatu baada ya kufanya hilo agano nao, walisikia habari ya kuwa watu hao ni jirani zao, na ya kwamba waliketi kati yao. Kisha wana wa Israeli walisafiri, wakaifikilia miji ya watu hao siku ya tatu. Basi miji ya watu hao ilikuwa ni hii, Gibeoni, na Kefira, na Beerothi, na Kiriath-yearimu. Wana wa Israeli hawakuwapiga, kwa sababu wakuu wa mkutano walikuwa wamekwisha kuwaapia kwa Bwana, Mungu wa Israeli. Nao mkutano wote wakawanung'unikia hao wakuu. Lakini wakuu wote waliwaambia mkutano wote, Sisi tumewaapia kwa Bwana, Mungu wa Israeli; basi sasa hatuwezi kuwagusa watu hawa. Tutawafanyia neno hili, kisha tutawaacha wawe hai; hasira isije juu yetu, kwa ajili ya hicho kiapo tulichowaapia.Wakuu waliwaambia, Waacheni wawe hai; basi wakawa wenye kupasua kuni, na wenye kuteka maji, kwa ajili ya mkutano wote; vile vile kama hao wakuu walivyowaambia. Basi Yoshua akawaita, akanena nao, na kuwaambia, Mbona ninyi mmetudanganya, huku mkisema, Sisi tu mbali sana na ninyi; nanyi kumbe! Mwakaa kati yetu? Basi sasa mmelaaniwa kisha hatakosekana kuwapo mtu wa kwenu aliye mtumwa, wenye kupasua kuni, na wenye kuteka maji, kwa ajili ya nyumba ya Mungu wangu. Nao wakamjibu Yoshua, na kusema, Ni kwa sababu ya sisi watumishi wako kuambiwa hakika, jinsi huyo Bwana, Mungu wako alivyomwamuru mtumishi wake Musa kuwapa ninyi nchi hii yote, na kuwaangamiza wenyeji wote wa nchi hii watoke mbele zenu; kwa sababu hii tuliogopa mno kwa ajili ya uhai wetu kwa sababu yenu, nasi tumefanya neno hili. Basi sasa, tazama, sisi tu mkononi mwako; basi kama uonavyo kuwa ni vyema na haki kwako wewe kututenda, tutende vivyo. Naye akawafanyia hivyo, na kuwaokoa na mkono wa wana wa Israeli, ili wasiwaue. Siku iyo hiyo Yoshua akawafanya kuwa ni wenye kupasua kuni, na wenye kuteka maji, kwa ajili ya mkutano, na kwa ajili ya madhabahu ya Bwana, hata siku hii ya leo, katika mahali hapo atakapopachagua.”            

Israel walifanya agano na Wagibeoni bila kujua kuwa wagibeoni waliishi Kanaani na kuwa waliwadanganya Israel baadaye walipogundua waliwajibika kuwalinda kwa sababu waliapa kuwa na amani nao na kama wangeliwaua ingewagharimu Israeli kufa au kupata madhara kutoka kwa Mungu kwa sababu ya agano hilo, wakati fulani Sauli Mfalme wa Israel aliuwa baadhi wa wagibeoni kinyume na agano hili na madhara makubwa yaliipata  Israel na familia yake hata wakati wa utawala wa Daudi

2Samuel 21:1-9 ”Kulikuwa na njaa siku za Daudi muda wa miaka mitatu, mwaka kwa mwaka; naye Daudi akautafuta uso wa Bwana. Bwana akasema, Ni kwa ajili ya Sauli, na kwa nyumba yake yenye damu, kwa kuwa aliwaua hao Wagibeoni. Ndipo mfalme akawaita Wagibeoni akawaambia; (basi Wagibeoni si wa wana wa Israeli, ila ni wa masalio ya Waamori; na wana wa Israeli walikuwa wamewaapia; lakini Sauli akatafuta kuwaua katika juhudi yake kwa ajili ya wana wa Israeli na Yuda;) basi Daudi akawaambia hao Wagibeoni, Niwatendee nini? Na kwa tendo gani nifanye upatanisho, mpate kuubariki urithi wa Bwana? Na hao Wagibeoni wakamwambia, Si jambo la fedha wala dhahabu lililo kati ya sisi na Sauli, au nyumba yake; wala si juu yetu kumwua mtu ye yote katika Israeli. Akasema Mtakayoyanena, ndiyo nitakayowatendea ninyi. Wakamwambia mfalme, Yule mtu aliyetupoteza, na kutufanyia shauri la kutuharibu, tusikae katika mipaka yo yote ya Israeli, basi, na tutolewe watu saba katika wanawe, nasi tutawatundika mbele za Bwana katika Gibeoni, katika mlima wa Bwana. Mfalme akasema, Nitawatoa. Lakini mfalme akamwachilia Mefiboshethi, mwana wa Yonathani, mwana wa Sauli, kwa ajili ya kiapo cha Bwana kilichokuwa kati yao, yaani, kati ya Daudi na Yonathani, mwana wa Sauli. Ila mfalme akawatwaa hao wana wawili wa Rispa, binti Aya, aliomzalia Sauli, Armoni na Mefiboshethi; na wana watano wa Merabu binti Sauli, aliomzalia Adrieli, mwana wa Barzilai, Mmeholathi; akawatia mikononi mwa Wagibeoni, nao wakawatundika mlimani mbele za Bwana, nao wakaangamia wote saba pamoja; wakauawa siku za mavuno, za kwanza, mwanzo wa mavuno ya shayiri.”   

Kwa hiyo wote tumeona na kufahamu na kutambua kuhusu agano sasa kwa bahati mbaya au njema ndoa zote za watu wa Mungu huangukia katika sifa za kuwa na agano, sio patano, sio mkataba, wala sio nadhiri, kwa sababu hiyo mwanandoa awaye yote anapomtendea mwenzake mambo ya hiyana anavunja agano, mfano kama mwanamke anamnyima mumewe tendo la ndoa pasipo sababu za msingi analivunja agano na kwa sababu hiyo anapaswa kufa na hatouawa na mwanadamu bali atauawa na Mungu mwenyewe, au anaweza kupata madhara makubwa na yakamgharimu sana na mwanamke akimuacha mkewe au watu hao wakitalikiana wanalivunja agano na yule ambaye ndiye chanzo au sababu ya mgogoro huo kifo kinamuhusu na yeye aliye sababu za mwanzoni za kupelekea agano kuharibika atatangulia kufa ni kwa sababu kama hizo Neno la Mungu linatahadharisha wanandoa kutokufanyiana mambo ya hiyana kinyume na kile kilichoahidiwa katika maandiko ona :-

Malaki 2:13-16 ”Tena mnatenda haya nayo; mnaifunikiza madhabahu ya Bwana kwa machozi, kwa kulia na kwa kuugua, hata asiiangalie tena hiyo dhabihu, wala kuitakabali mikononi mwenu na kuiridhia. Lakini ninyi mwasema, Ni kwa sababu gani? Ni kwa sababu Bwana amekuwa shahidi kati ya wewe na mke wa ujana wako, uliyemtenda mambo ya hiana, angawa yeye ni mwenzako, na mke wa agano lako. Hakuna mtu mmoja aliyetenda hivi, ambaye alikuwa na ufahamu kidogo. Au je! Kuna mtu mmoja atafutaye mzao mwenye kumcha Mungu? Kwa hiyo jihadharini roho zenu; mtu awaye yote asimtende mke wa ujana wake mambo ya hiana. Maana mimi nakuchukia kuachana, asema Bwana, Mungu wa Israeli; naye aifunikizaye nguo yake kwa udhalimu namchukia, asema Bwana wa majeshi; basi jihadharini roho zenu, msije mkatenda kwa hiana.”

1Wakorintho 7:3-5 ”Mume na ampe mkewe haki yake, na vivyo hivyo mke na ampe mumewe haki yake. Mke hana amri juu ya mwili wake, bali mumewe; vivyo hivyo mume hana amri juu ya mwili wake, bali mkewe. Msinyimane isipokuwa mmepatana kwa muda, ili mpate faragha kwa kusali; mkajiane tena, Shetani asije akawajaribu kwa kutokuwa na kiasi kwenu.”

Waebrania 13:4 ”Ndoa na iheshimiwe na watu wote, na malazi yawe safi; kwa maana waasherati na wazinzi Mungu atawahukumia adhabu.”

Watu wengi hawafahamu kuwa kunyimana tendo la ndoa ni kuvunja agano la ndoa, katika vitu ambavyo huwaunganisha wanandoa na kuwafanya waache kila kitu kwa wazazi wao ni pamoja na tendo la ndoa, lakini kwa bahati mbaya watu wengi hunyimana tendo la ndoa huku wakilitumia tendo hilo kama fimbo ya kuadhibiana na kusahau kuwa waliapa mbele za Mungu na mashahidi wake na wakiwa hawajui kama ni kosa na ni uvunjifu wa ukiukwaji wa haki za agano, aidha kama wana ndoa hao pia watafanya uasherati na zinaa Mungu atawahukumia adhabu kwa sababu wanalivunja agano na kusababisha madhara makubwa sio kwa familia na ndoa pekee lakini pia kwa ardhi na inchi na kufanya mambo kuwa magumu sana. Kwa ujumla kuvunja agano lolote lile liwe la kimila au linalomuhusisha Mungu kiroho ni jambo baya sana na lina madhara makubwa! Na mara nyingi sana wanadamu walipovunja agano la Mungu Mungu aliilaani ardhi kwaajili yao ili kusababisha madhara juu yao na kizazi chao

Mwanzo 3:17-19 ”Akamwambia Adamu, Kwa kuwa umeisikiliza sauti ya mke wako, ukala matunda ya mti ambao nalikuagiza, nikisema, Usiyale; ardhi imelaaniwa kwa ajili yako; kwa uchungu utakula mazao yake siku zote za maisha yako; michongoma na miiba itakuzalia, nawe utakula mboga za kondeni; kwa jasho la uso wako utakula chakula, hata utakapoirudia ardhi, ambayo katika hiyo ulitwaliwa; kwa maana u mavumbi wewe, nawe mavumbini utarudi.”

Mwanzo 4:10-14 ”Akasema, Umefanya nini? Sauti ya damu ya ndugu yako inanililia kutoka katika ardhi. Basi sasa, umelaaniwa wewe katika ardhi, iliyofumbua kinywa chake ipokee damu ya ndugu yako kwa mkono wako; utakapoilima ardhi haitakupa mazao yake; utakuwa mtoro na mtu asiye na kikao duniani. Kaini akamwambia BWANA, Adhabu yangu imenikulia kubwa, haichukuliki. Tazama, umenifukuza leo katika uso wa ardhi, nitasitirika mbali na uso wako, nami nitakuwa mtoro na mtu asiye na kikao duniani; hata itakuwa kila anionaye ataniua. ”

Unaweza kuona kuwa mara nyingi sana Mwanadamu alipokosea na kutenda dhambi ya kuvunja agano au kuua Mungu aliilaani ardhi hii ni kwa sababu kadhaa za muhimu za kiroho na kimaandiko, kuvunja agano au kuua na kumwaga damu juu ya nchi na dhambi nyinginezo zote huathiri chanzo cha asili ya mwanadamu

Mwanadamu alitoka katika mavumbi ya ardhi kwa hiyo uko uhusiano wa karibu sana kati ya ardhi na mwanadamu, ardhi ni mama wa mwanadamu na madhara ya dhambi hukimbilia katika ardhi ambayo ni chanzo cha uhai wako, ardhi inakuwa ngumu kukunufaisha, ardhi inakukataa na kusababisha ugumu wa maisha na kutokufanikiwa na zaidi sana kupunguza uwezekano wa kuishi siku nyingi, ardhi inapolaaniwa kwaajili yako maana yake unaongezewa ugumu wa maisha na kupunguziwa siku zako za kuishi

Mwanzo 2:7 ”BWANA Mungu akamfanya mtu kwa mavumbi ya ardhi, akampulizia puani pumzi ya uhai; mtu akawa nafsi hai.”

Mungu alimpa mwanadamu ardhi, ardhi ndio eneo la utawala wa mwanadamu, ni katika ardhi ndiko kunakotkea mafanikio yetu yote ya kimwili, utajiri wa kila kitu uko ardhini kwa hiyo mwanadamu alitakiwa kuitawala ardhi na kuitunza na kuilima kwa hiyo mwanadamu anapotenda dhambi ikiwa ni pamoja na kuvunja agano laana hukimbilia katika ardhi ili kuifanya kazi ya mwanadamu kuwa ngumu sana Zaburi 115:16 ” Mbingu ni mbingu za Bwana, Bali nchi amewapa wanadamu.”

Mwanzo 1:28 ”Mungu akawabarikia, Mungu akawaambia, Zaeni, mkaongezeke, mkaijaze nchi, na kuitiisha; mkatawale samaki wa baharini, na ndege wa angani, na kila kiumbe chenye uhai kiendacho juu ya nchi. Mungu akasema, Tazama, nimewapa kila mche utoao mbegu, ulio juu ya uso wa nchi yote pia, na kila mti, ambao matunda yake yana mbegu; vitakuwa ndivyo chakula chenu; na chakula cha kila mnyama wa nchi, na cha kila ndege wa angani, na cha kila kitu kitambaacho juu ya nchi, chenye uhai; majani yote ya miche, ndiyo chakula chenu; ikawa hivyo.”

Ardhi ndiyominayobeba baraka za wanadamu na ndiyo inayobeba laana za wanadamu, wanadamu wanapofanya dhambi na dhuluma na kuvunja maagano yaani zinaa nchi ndiyo inayoomboleza kwa hiyo madhara ya dhambi hubebwa na ardhi au nchi ile

Yeremia 23:10 ” Maana nchi imejaa wazinzi; kwa sababu ya kuapa nchi inaomboleza; malisho ya nyikani yamekauka; mwenendo wao ni mbaya, na nguvu zao si za haki.”

Kuvunja maagano kumesababisha laana na maisha magumu sana katika jamii na kutokufanikiwa na kutokupata ufumbuzi kwa sababu aliyekosewa na Mungu mwenyewe aliye shahidi wa maagano yanayovunjwa kila iitwapo leo, karibu laana zote zinazowapata wanadamu zinaungamanishwa na ardhi

Kumbukumbu 28:15-20 ”Lakini itakuwa usipotaka kuisikiza sauti ya Bwana, Mungu wako, usiyaangalie kufanya maagizo yake yote na amri zake, nikuagizazo hivi leo, ndipo zitakapokujia laana hizi zote na kukupata. Utalaaniwa mjini, utalaaniwa na mashambani. Litalaaniwa kapu lako na chombo chako cha kukandia. Utalaaniwa uzao wa tumbo lako, na uzao wa nchi yako, maongeo ya ng'ombe wako, na wadogo wa kondoo zako. Utalaaniwa uingiapo, utalaaniwa na utokapo, Bwana atakuletea laana na mashaka, na kukemewa, katika yote utakayotia mkono wako kuyafanya, hata uangamie na kupotea kwa upesi; kwa ule uovu wa matendo yako, uliyoniacha kwayo.”

Madhara ya kuvunja agano

Kuvunja agano kuna madhara makubwa sana  na kunasababisha laana na hukumu ya Mungu ambayo kilele chake ni kifo na kama utaishi utaishi maisha ya taabu sana, na kula mkate wa shida, wakati mwingine madhara ya kuvunja agano yanaweza kuathiri sio mtu mmoja tu bali na jamii yake ni ukweli ulio wazi kuwa hata watu wa Musa, walionywa kuwa laana ya Mungu ingembatana na wale wasiotii na wenye kulivunja agano la Mungu kwa hiyo kuna madhara makubwa sana na nilimuelewa kijana yule wa kimaasai aliposema sisi tunaogopa kuvunja agano! Hapa yako madhara yanayoambatana na kuvunjwa kwa agano, huku masaini kila changamoto inapotokea wamasai hukimbilia kuchinja mwana kondoo kwaajili ya kuondoa laana katika ardhi, hata hivyo sisi tunayo damu ya Yesu ambayo huvunja na kuharibu laana zote na kutunenea mema kama damu ya Habili.

1.      Kuvunja agano kunakaribisha hukumu ya Mungu

 

Kumbukumbu 28:15-67 “Lakini itakuwa usipotaka kuisikiza sauti ya Bwana, Mungu wako, usiyaangalie kufanya maagizo yake yote na amri zake, nikuagizazo hivi leo, ndipo zitakapokujia laana hizi zote na kukupata. Utalaaniwa mjini, utalaaniwa na mashambani. Litalaaniwa kapu lako na chombo chako cha kukandia. Utalaaniwa uzao wa tumbo lako, na uzao wa nchi yako, maongeo ya ng'ombe wako, na wadogo wa kondoo zako. Utalaaniwa uingiapo, utalaaniwa na utokapo, Bwana atakuletea laana na mashaka, na kukemewa, katika yote utakayotia mkono wako kuyafanya, hata uangamie na kupotea kwa upesi; kwa ule uovu wa matendo yako, uliyoniacha kwayo. Bwana atakuambatanisha na tauni, hata atakapokwisha kukuondoa katika nchi uingiayo kwa kuimiliki. Bwana atakupiga kwa kifua kikuu, na kwa homa, na kwa kuwashwa, na kwa hari ya moto, na kwa upanga, na kwa ukaufu, na kwa koga; navyo vitakufukuza hata uangamie. Na mbingu zako zilizo juu ya kichwa chako zitakuwa shaba, na nchi iliyo chini yako itakuwa chuma. Bwana atafanya mvua ya nchi yako iwe vumbi na mchanga; itakujilia juu yako kutoka mbinguni hata uangamie. Bwana atakufanya upigwe mbele ya adui zako; utawatokea juu yao kwa njia moja, lakini utakimbia mbele yao kwa njia saba; nawe utatupwa huko na huko katika falme zote za duniani. Na mzoga wako utakuwa chakula cha ndege wote wa angani, na wanyama wote wa duniani, pasiwe na mtu wa kuwafukuza. Bwana atakupiga kwa majipu ya Misri, na kwa bawasiri, na kwa pele, na kwa kujikuna, ambayo hupati kupoa. Bwana atakupiga kwa wazimu, na kwa upofu, na kwa bumbuazi la moyoni; utakwenda kwa kupapasa-papasa mchana, kama apapasavyo kipofu gizani, wala hufanikiwi katika njia zako; nawe sikuzote utaonewa na kutekwa nyara, wala hapatakuwa na mtu wa kukuokoa. Utaposa mke na mume mwingine atalala naye; utajenga nyumba usiikae; utapanda mizabibu usitumie matunda yake. Ng'ombe wako atachinjwa mbele ya macho yako, usile nyama yake; utanyang'anywa punda wako mbele ya uso wako kwa jeuri, usirudishiwe; kondoo zako watapewa adui zako, usipate mtu wa kukuokoa. Wanao na binti zako litapewa taifa lingine, na macho yako yataangalia, na kuzimia kwa kuwatamani mchana kutwa; wala hapatakuwa na kitu katika uwezo wa mkono wako. Matunda ya nchi yako, na taabu yako yote, vitaliwa na taifa usilolijua; utaonewa tu, na kupondwa chini daima; hata uwe mwenye wazimu kwa yaonwayo na macho yako, utakayoyaona. Bwana atakupiga magoti na miguu kwa jipu lililo zito, usilopata kupozwa, tokea wayo wa mguu mpaka utosi wa kichwa. Bwana atakupeleka wewe, na mfalme wako utakayemweka juu yako, kwa taifa usilolijua wewe wala baba zako; nawe huko utatumikia miungu mingine ya miti na mawe. Nawe utakuwa ushangao, na mithali, na dharau, kati ya mataifa yote huko atakakokuongoza Bwana. Mbegu nyingi utazichukua nje shambani, lakini utavuna haba, kwa kuwa nzige watazila. Utapanda mizabibu na kuitengeza, wala hutakunywa katika divai yake, wala kuichuma kwani italiwa na mabuu. Utakuwa na mizeituni katika mipaka yako yote usijipake mafuta yake; kwa kuwa mzeituni wako utapukutika. Utazaa wana na binti, lakini hawatakuwa wako wewe; kwa sababu watakwenda utumwani. Miti yako yote, na mazao ya nchi yako, nzige watakuwa nayo. Mgeni aliye kati yako atazidi kupaa juu yako; nawe utazidi kushuka chini. Yeye atakukopesha, wala wewe usimkopeshe; yeye atakuwa ni kichwa, wewe utakuwa mkia. Na laana hizi zote zitakujilia juu yako, zitakuandama na kukupata, hata uangamizwe, kwa kuwa hukuisikiza sauti ya Bwana, Mungu wako, kushika maagizo yake na amri zake alizokuagiza; nazo zitakuwa juu yako kwa ishara na ajabu, na juu ya uzao wako milele; kwa kuwa hukumtumikia Bwana, Mungu wako, kwa furaha na moyo wa kushukuru, kwa ajili ya ule wingi wa vitu vyote; kwa hiyo utawatumikia adui zako atakaowaleta Bwana juu yako, kwa njaa, na kwa kiu, na kwa uchi, na kwa uhitaji wa vitu vyote; naye atakuvika kongwa la chuma shingoni mwako, hata atakapokwisha kukuangamiza. Bwana atakuletea taifa juu yako kutoka mbali, kutoka ncha ya dunia, kama arukavyo tai; taifa usiloufahamu ulimi wake; taifa lenye uso mkali, ambalo haliangalii uso wa mzee, wala halipendelei kijana; naye atakula uzao wa ng'ombe wako wa mifugo, na uzao wa nchi yako mpaka utakapokwisha kuangamizwa; wala hatakuachia nafaka, wala divai, wala mafuta, wala maongeo ya ng'ombe wako, wala wana-kondoo wako, hata atakapokwisha kukuangamiza. Naye atakuhusuru katika malango yako yote, hata kuta zako ndefu, zenye maboma, ulizokuwa ukiziamini, zishuke, katika nchi yako yote kila upande; naye atakuhusuru katika malango yako yote kila upande, katika nchi yako yote aliyokupa Bwana, Mungu wako. Nawe utakula uzao wa tumbo lako mwenyewe, nyama ya wana wako na binti zako aliokupa Bwana, Mungu wako; katika mazingirwa na katika mkazo utakaokazwa na adui zako. Mtu mume kati yenu aliye mwororo na laini sana, jicho lake litakuwa ovu juu ya nduguye, na juu ya mke wa kifuani mwake, na juu ya masalio ya wanawe waliosalia naye; hata asitake wao mmojawapo apewe katika nyama ya wanawe atakaowala, kwa kuwa hana kitu kilichomsalia kwake; katika mazingirwa na mkazo utakaokazwa na adui yako katika malango yako yote. Mwanamke kati yenu aliye mwororo na laini, ambaye hangehatirisha kuweka wayo wa mguu wake nchi kwa umalidadi na ulaini, jicho lake huyu litakuwa ovu juu ya mume wa kifuani mwake, na juu ya mwanawe, na juu ya binti yake, na juu ya mchanga wake atokaye katikati ya miguu yake, na juu ya wanawe atakaowazaa; kwa kuwa atawala kwa siri, kwa uhitaji wa vitu vyote; katika mazingirwa na mkazo utakaokazwa na adui yako katika malango yako. Kama hutaki kutunza kufanya maneno yote ya torati hii yaliyoandikwa katika kitabu hiki, upate kulicha jina hili la fahari na utisho, Bwana, MUNGU WAKO; ndipo atakapofanya Bwana mapigo yako yawe ya ajabu, na mapigo ya uzao wako, mapigo makubwa kwa kweli, ya kudumu sana, na magonjwa mazito ya kudumu sana. Naye atakurejezea maradhi yote ya Misri juu yako uliyokuwa ukiyaogopa, nayo yataambatana nawe. Tena kila ugonjwa, na kila pigo yasiyoandikwa katika kitabu cha torati hii, atakutia nayo Bwana juu yako, hata utakapokwisha kuangamizwa. Nanyi mtasalia wachache kwa hesabu, ninyi mliokuwa mfano wa nyota za mbinguni kwa wingi; kwa kuwa hukuisikiza sauti ya Bwana, Mungu wako.Tena itakuwa, kama vile alivyokuwa akifurahi Bwana juu yenu kwa kuwatendea mema na kuwafanya kuwa wengi, ndivyo atakavyofurahi Bwana juu yenu kwa kuwapoteza na kuwaangamiza; nanyi mtanyakuliwa katika hiyo nchi mwingiayo kuimiliki.Bwana atakutawanya katika mataifa yote, tokea ncha hii ya dunia hata ncha hii ya dunia; nawe huko utatumikia miungu mingine usiyoijua wewe wala baba zako, nayo ni miti na mawe. Wala katika mataifa hayo hutapata raha iwayo yote, wala hutakuwa na kituo cha wayo wa mguu wako; lakini Bwana atakupa huko moyo wa kutetema, na macho ya kuzimia, na roho ya kudhoofika; na uzima wako utakuwa na wasiwasi mbele yako; nawe utakuwa na woga usiku na mchana, wala hutaamini kamwe maisha yako; asubuhi utasema, Laiti ingekuwa jioni! Na jioni utasema, Laiti ingekuwa asubuhi! Kwa kicho cha moyo wako utakavyokucha, na kuona kwa macho yako utakavyoona.”

 

2.      Kuvunja agano kunakufanya utengwe na Mungu

 

Kuvunja agano kunasababisha mtu utengwe kiroho na Mungu, jambo litakalopelekea upoteze Baraka na ulinzi wa Mungu

 

Yeremia 31:31-33 “Angalia, siku zinakuja, asema Bwana, nitakapofanya agano jipya na nyumba ya Israeli, na nyumba ya Yuda. Si kwa mfano wa agano lile nililolifanya na baba zao, katika siku ile nilipowashika mkono, ili kuwatoa katika nchi ya Misri; ambalo agano langu hilo walilivunja, ingawa nalikuwa mume kwao, asema Bwana. Bali agano hili ndilo nitakalofanya na nyumba ya Israeli, baada ya siku zile, asema Bwana; Nitatia sheria yangu ndani yao, na katika mioyo yao nitaiandika; nami nitakuwa Mungu wao, nao watakuwa watu wangu.

 

Katika kifungu hiki cha maandiko Mungu anakumbuika na kusikitika kuwa Israel walilivunja agano agano lake na kwa sababu hiyo hii ilisababisha watengwe na Mungu na kupelekwa utumwani huko Babeli, Hakuna jambo baya duniani kama kutengwa na uso wa Mungu, Ulinzi wake unaondoka na unakabiliwa na uonevu na kila atakayekuona atakuua tu

 

Mwanzo 4:13-14 “Kaini akamwambia BWANA, Adhabu yangu imenikulia kubwa, haichukuliki.Tazama, umenifukuza leo katika uso wa ardhi, nitasitirika mbali na uso wako, nami nitakuwa mtoro na mtu asiye na kikao duniani; hata itakuwa kila anionaye ataniua.”    

 

3.      Kuvunja agano husababisha laana na adhabu kali

 

Kwa ujumla kuvunja aano kunasababisha madhara makubwa sana ikiwemo kupoteza Baraka, kupelekwa utumwani, kutengwa kiroho na Mungu, hukumu mbaa, kwa ujumla kuna adhabu kali sana zinazoambatana na laana na madhara mbalimbali

 

Walawi 26:14-16 “Mtoe huyo aliyeapiza nje ya marago; na wale wote waliomsikia na waweke mikono yao kichwani mwake, kisha mkutano wote na wamwue kwa kumpiga kwa mawe. Nawe nena na wana wa Israeli na kuwaambia, Mtu awaye yote atakayemlaani Mungu wake atachukua dhambi yake. Na yeye atakayelikufuru jina la BWANA hakika atauawa; mkutano wote watamwua kwa kumpiga kwa mawe; kama ni mgeni, kama ni mzalia, hapo atakapolikufuru jina la BWANA atauawa.”

 

4.      Kuvunja agano kunasababisha Magonjwa, laana na utasa na kushindwa vita

 

Yeremia 34:18-20 “Na watu hao waliolivunja agano langu, wasioyatimiza maneno ya agano lile, walilolifanya mbele zangu, wakati ule walipomkata ndama vipande viwili, wakapita katikati ya vipande vile; wakuu wa Yuda, na wakuu wa Yerusalemu, matowashi, na makuhani, na watu wote wa nchi, waliopita katikati ya vipande vile vya huyo ndama; mimi nitawatia katika mikono ya adui zao, na katika mikono ya watu wale wanaowatafuta roho zao, na mizoga yao itakuwa ni chakula cha ndege za mbinguni, na cha wanyama wakali wa nchi.”

 

Agano la Mungu linaposhikwa kwa uaminifu husababisha Baraka mbalimbali ikiwepo, Baraka ya uzao, kubarikiwa mashambani, kupewa ushindi vitani, kuwa na nguvu dhidi ya maadui zako, na mengineyo mengi, lakini linapovunjwa hali huwa tofauti, utatiwa mikononi mwa adui zako, utaonewa, utapata utasa, utakosa uzao, hali itakuwa mbaya kila eneo la maisha yako, maswala ya maisha yako mengi na milango ya Baraka mingi itafungwa

 

Mungu ataachilia laana za kila aina kwa wale wanaokosa uaminifu kwa agano walilolifanya mbele zake, kumbuka kuwa inaweza kuchukua muda mrefu sana kuona hali hiyo kwa sababu Mungu sio mwepesi wa hasira lakini hata hivyo hawezi kuvumilia hata mwisho na kukuacha bila madhara endapo umekuwa mstari wa mbele kuvunja agano lake, na kama ulikuwa hujagundua mpaka utakapokuja kugundua utakuwa umeshateseka sana   

           

Mifano ya watu waliovunja agano na kupata madhara

Kuvunja agano ni kosa kubwa sana linaloharibu haki na utakatifu wa Mungu, ni udhalilishaji mkubwa sana kwa upande wa Mungu ambaye anatazamia, umakini mkubwa wa uaminifu katika makubaliano baina yetu na yeye, Maandiko yanaonyesha kuwa kuna madhara makubwa sana yanayowapata watu wanapovunja maagano na kusababisha madhara na changamoto kubwa na za kudumu, Mungu ni kweli ni mwingi wa huruma na rehema na neema lakini vile vile ni Mungu wa haki, hawezi kuachilia dhuluma itawale akiwa yeye ni mwenye haki.

Mwanzo 18:25 “Hasha usifanye hivyo, ukamwue mwenye haki pamoja na mwovu, mwenye haki awe kama mwovu. Hasha; Mhukumu ulimwengu wote asitende haki?

1.      Adam na Eva – walikuwa na agano na Mungu ambalo lilistawishwa katika bustani ya Edeni ambapo Mungu aliwataka wasile kutoka katika mti wa ujuzi wa mema na mabaya lakini katika hali isiyokuwa ya kawaida Adam na Eva walikula tunda walilokatazwa na haraka sana kuvunjwa kwa agano lile kulipelekea kuweko kwa madhara makubwa sana, kifo cha kiroho, kufukuzwa kutoka katika uwepo wa Mungu na Bustani ya Edeni, kuzaa kwa uchungu, kula kwa jasho, kuzaliwa kwa michongoma, kulaaniwa kwa ardhi, na  kifo haya yakawa ni madhara ya kudumu kutoka kwa Adamu na hata uzao wake hata leo

 

Mwanzo 3:16-19 “Akamwambia mwanamke, Hakika nitakuzidishia uchungu wako, na kuzaa kwako; kwa utungu utazaa watoto; na tamaa yako itakuwa kwa mumeo, naye atakutawala. Akamwambia Adamu, Kwa kuwa umeisikiliza sauti ya mke wako, ukala matunda ya mti ambao nalikuagiza, nikisema, Usiyale; ardhi imelaaniwa kwa ajili yako; kwa uchungu utakula mazao yake siku zote za maisha yako; michongoma na miiba itakuzalia, nawe utakula mboga za kondeni; kwa jasho la uso wako utakula chakula, hata utakapoirudia ardhi, ambayo katika hiyo ulitwaliwa; kwa maana u mavumbi wewe, nawe mavumbini utarudi.”        

 

2.      Wana wa Israel – Walipewa agano na Mungu kupitia Musa mtumishi wake katika mlima wa Sinai, lakini mara kwa mara wana wa Israel walilivunja agano hilo kwa kuabudu miungu jambo ambalo mara kwa mara lilisababisha mapigo na kuchelewa kuingia katika nchi ya kanaani kwa miaka 40

 

Kutoka 32:31-35 “Musa akarejea kwa BWANA akasema, Aa! Watu hawa wametenda dhambi kuu wamejifanyia miungu ya dhahabu. Walakini sasa, ikiwa utawasamehe dhambi yao na kama sivyo, unifute, nakusihi, katika kitabu chako ulichoandika. BWANA akamwambia Musa, Mtu ye yote aliyenitenda dhambi ndiye nitakayemfuta katika kitabu changu. Basi sasa uende ukawaongoze watu hawa mpaka mahali pale ambapo nimekwambia habari zake; tazama, malaika wangu atakutangulia; pamoja na hayo siku nitakayowajilia nitawapatiliza kwa ajili ya dhambi yao. BWANA akawapiga hao watu, kwa walivyoifanya ile ndama, ambayo Haruni aliifanya.”

 

3.      Mfalme Sauli kwa kuwaua wagibeoni – Aliweza kusababisha madhara ya kuuawa kwa watoto wake saba, kwa sababu aliwaua  Wagibeoni na kusahau kuwa Israel walikuwa wamefanya nao agano na Mungu ni Mungu ashikaye maagano

 

2Samuel 1-9 “Kulikuwa na njaa siku za Daudi muda wa miaka mitatu, mwaka kwa mwaka; naye Daudi akautafuta uso wa Bwana. Bwana akasema, Ni kwa ajili ya Sauli, na kwa nyumba yake yenye damu, kwa kuwa aliwaua hao Wagibeoni. Ndipo mfalme akawaita Wagibeoni akawaambia; (basi Wagibeoni si wa wana wa Israeli, ila ni wa masalio ya Waamori; na wana wa Israeli walikuwa wamewaapia; lakini Sauli akatafuta kuwaua katika juhudi yake kwa ajili ya wana wa Israeli na Yuda;) basi Daudi akawaambia hao Wagibeoni, Niwatendee nini? Na kwa tendo gani nifanye upatanisho, mpate kuubariki urithi wa Bwana? Na hao Wagibeoni wakamwambia, Si jambo la fedha wala dhahabu lililo kati ya sisi na Sauli, au nyumba yake; wala si juu yetu kumwua mtu ye yote katika Israeli. Akasema Mtakayoyanena, ndiyo nitakayowatendea ninyi. Wakamwambia mfalme, Yule mtu aliyetupoteza, na kutufanyia shauri la kutuharibu, tusikae katika mipaka yo yote ya Israeli, basi, na tutolewe watu saba katika wanawe, nasi tutawatundika mbele za Bwana katika Gibeoni, katika mlima wa Bwana. Mfalme akasema, Nitawatoa. Lakini mfalme akamwachilia Mefiboshethi, mwana wa Yonathani, mwana wa Sauli, kwa ajili ya kiapo cha Bwana kilichokuwa kati yao, yaani, kati ya Daudi na Yonathani, mwana wa Sauli. Ila mfalme akawatwaa hao wana wawili wa Rispa, binti Aya, aliomzalia Sauli, Armoni na Mefiboshethi; na wana watano wa Merabu binti Sauli, aliomzalia Adrieli, mwana wa Barzilai, Mmeholathi; akawatia mikononi mwa Wagibeoni, nao wakawatundika mlimani mbele za Bwana, nao wakaangamia wote saba pamoja; wakauawa siku za mavuno, za kwanza, mwanzo wa mavuno ya shayiri.”

Kwa ujumla kuvunja maagano kuna madhara makubwa sana na kunaleta laana juu ya nchi, maisha na mwenendo mzima wa watu, hapa ni maagano ya namna zote likiwepo agano la ndoa, linapovunjwa agano la aina yoyote ambalo kwalo Mungu ni shahidi ni ukweli ulio wazi kuwa kunakuwa na madhara makubwa sana kwa kuvunjwa kwa agano hilo kwa sababu Mungu ni Mungu ashikaye maagano na alijulikana hivyo na watakatifu waliotutangulia. watakatifu waliotutangulia walimfahamu Mungu jinsi alivyo muaminifu katika kushika maagano  walipoomba, walimkumbusha Mungu sifa yake hii jinsi alivyo muaminifu katika kushika maagano walipoomba walimkumbusha Mungu ahadi alizojifunga kwao au kwa Baba zao Ibrahimu, Isaka na Yakobo, kuhusu Agano na rehema zake hii inapandisha sana imani kujua kuwa Mungu wetu ni Mungu muaminifu si muongo,

Hesabu 23:19. “Mungu si mtu, aseme uongo; Wala si mwanadamu, ajute; Iwapo amesema, hatalitenda? Iwapo amenena, hatalifikiliza?

Wanadamu ni waongo lakini Mungu si muongo wala si mwanadamu hata ajute Yeye akinena hutenda na ni muaminifu toka kizazi hata kizazi Fadhili zake zinadumu hata milele wakati mnapoweka Agano na mwenzi wako au na unapofanya agano lolote lile na yeye akawa ni shahidi basi fahamu ya kuwa agano hilo ukilivunja Mungu anakasirishwa na anapatiliza na madhara yake ni kifo.

Mambo ya kufanya unapokuwa umevunja agano

Rafiki yangu katika jamii ya kimasai aliniambia kuwa katika ardhi ya kimasai hakuna jambo linaogopewa kama laana, anasema katika jamii yetu hata mtu akiumizwa kiasi cha kutoa damu, wazee lazima watachinja kondoo kwaajili ya upatanishi na kuzuia laana, na vile vile kama mtu amevunja agano basi ni lazima achinje kondoo ili laana iwe mbali naye na pia ardhi iweze kubarikiwa! Wamasai wakati wote wanahakikisha kuwa ikiwezekana achinjwe kondoo au mbuzi kuhakikisha kuwa wao na inchi yao inakuwa salama, kwa bahati nzuri sisi sasa sisi tunayo Damu ya Yesu Kristo ambayo imemwagika msalabani na ina nguvu na uwezo wa kutuokoa na laana na dhambi kama tutamwendea yeye kwa toba na kufanya mapinduzi makubwa ya kugeuzwa nia zetu na kuiitia damu ya Yesu yenye nguvu ya kutakasa kutuondolea changamoto zinazotukabili.

Waebrania 9:11-15 “Lakini Kristo akiisha kuja, aliye kuhani mkuu wa mambo mema yatakayokuwapo, kwa hema iliyo kubwa na kamilifu zaidi, isiyofanyika kwa mikono, maana yake, isiyo ya ulimwengu huu, wala si kwa damu ya mbuzi na ndama, bali kwa damu yake mwenyewe aliingia mara moja tu katika Patakatifu, akiisha kupata ukombozi wa milele. Kwa maana, ikiwa damu ya mbuzi na mafahali na majivu ya ndama ya ng'ombe waliyonyunyiziwa wenye uchafu hutakasa hata kuusafisha mwili; basi si zaidi damu yake Kristo, ambaye kwamba kwa Roho wa milele alijitoa nafsi yake kwa Mungu kuwa sadaka isiyo na mawaa, itawasafisha dhamiri zenu na matendo mafu, mpate kumwabudu Mungu aliye hai? Na kwa sababu hii ni mjumbe wa agano jipya, ili, mauti ikiisha kufanyika kwa kukomboa makosa yaliyokuwa chini ya agano la kwanza, hao walioitwa waipokee ahadi ya urithi wa milele     

Waebrania 10:1-10 “Basi torati, kwa kuwa ni kivuli cha mema yatakayokuwa, wala si sura yenyewe ya mambo hayo, kwa dhabihu zile zile wanazozitoa kila mwaka daima, haiwezi wakati wo wote kuwakamilisha wakaribiao. Kama ndivyo, je! Dhabihu hazingekoma kutolewa; kwa maana waabuduo, wakiisha kusafishwa mara moja, wasingejiona tena kuwa na dhambi? Lakini katika dhabihu hizo liko kumbukumbu la dhambi kila mwaka. Maana haiwezekani damu ya mafahali na mbuzi kuondoa dhambi. Kwa hiyo ajapo ulimwenguni, asema, Dhabihu na toleo hukutaka, Lakini mwili uliniwekea tayari; Sadaka za kuteketezwa na sadaka za dhambi hukupendezwa nazo; Ndipo niliposema, Tazama, nimekuja (katika gombo la chuo nimeandikiwa) Niyafanye mapenzi yako, Mungu. Hapo juu asemapo, Dhabihu na matoleo na sadaka za kuteketezwa na hizo za dhambi hukuzitaka, wala hukupendezwa nazo (zitolewazo kama ilivyoamuru torati), ndipo aliposema, Tazama, nimekuja niyafanye mapenzi yako. Aondoa la kwanza, ili kusudi alisimamishe la pili. Katika mapenzi hayo mmepata utakaso, kwa kutolewa mwili wa Yesu Kristo mara moja tu.”

Iwapo umejiingiza katika swala zima la kuharibu maagano haya ndiyo yakupasayo kufanya

1.      Tambua kuwa umeharibu agano – hatua ya kwanza ni lazima utambue ya kuwa umeharibu umevunja agano na kukubali kuwa umefanya upumbavu kwa kuvunja maagano ya Bwana, hii itajumuisha kujitathimini na kujitambua na kuanza kujutia huku ukimwambia Mungu dhambi ya kuvunja agano

 

1Wafalme 19:9-10. “Akafika kunako pango, akalala ndani yake. Na tazama, neno la Bwana likamjia, naye akamwambia, Unafanya nini hapa, Eliya? Akasema, Nimeona wivu mwingi kwa ajili ya Bwana Mungu wa majeshi; kwa kuwa wana wa Israeli wameyaacha maagano yako, na kuzivunja madhabahu zako, na kuwaua manabii wako kwa upanga; nami nimesalia, mimi peke yangu; nao wanitafuta roho yangu, waiondoe.”

 

Hosea 6:6-7 “Maana nataka fadhili wala si sadaka; na kumjua Mungu kuliko sadaka za kuteketezwa. Lakini wao wamelivunja hilo agano kama Adamu; huko wamenitenda mambo ya hiana.”

 

Yeremia 11:10 “Wameyarudia maovu ya baba zao, waliokataa kusikia maneno yangu; wamewafuata miungu mingine na kuwatumikia; nyumba ya Israeli, na nyumba ya Yuda, wameyavunja maagano yangu niliyoyafanya na baba zao. Basi, Bwana asema hivi, Tazama, nitaleta mabaya juu yao, ambayo hawataweza kuyakimbia; nao watanililia, walakini sitawasikiliza.”

 

Daniel 9:3-11 “Nikamwelekezea Bwana Mungu uso wangu, ili kutaka kwa maombi, na dua, pamoja na kufunga, na kuvaa nguo za magunia na majivu. Nikamwomba Bwana, Mungu wangu, nikaungama, nikasema, Ee Bwana, Mungu mkuu, mwenye kutisha, ashikaye maagano na rehema kwao wampendao, na kuzishika amri zake; tumefanya dhambi, tumefanya ukaidi, tumetenda maovu, tumeasi, naam, hata kwa kuyaacha maagizo yako na hukumu zako; wala hatukuwasikiliza watumishi wako, manabii, ambao kwa jina lako walisema na wafalme wetu, na wakuu wetu, na baba zetu, na watu wote wa nchi. Ee Bwana, haki ina wewe, lakini kwetu sisi kuna haya ya uso, kama hivi leo; kwa watu wa Yuda, na kwa wenyeji wa Yerusalemu, na kwa Israeli wote, walio karibu na hao walio mbali, katika nchi zote ulikowafukuza, kwa sababu ya makosa yao waliyokukosa.Ee Bwana, kwetu sisi kuna haya ya uso, kwa wafalme wetu, na wakuu wetu, na baba zetu, kwa sababu tumekutenda dhambi. Rehema na msamaha ni kwa Bwana Mungu wetu, ingawa tumemwasi; wala hatukuitii sauti ya Bwana, Mungu wetu, kwa kwenda katika sheria zake, alizoziweka mbele yetu kwa kinywa cha watumishi wake, manabii. Naam, Israeli wote wameihalifu sheria yako, kwa kugeuka upande, wasiisikilize sauti yako; basi kwa hiyo laana imemwagwa juu yetu, na uapo ule ulioandikwa katika sheria ya Musa, mtumishi wa Mungu; kwa sababu tumemtenda dhambi.”

 

Baada ya kuwa umetafakari ni maagano gani umeyavunja na kujutia na kusikitika sasa unaweza kufanya toba.

 

2.      Tubu – kutubu maana yake ni kuadhimia au kudhamiria kugeuka, acha matendo yote yanayohusisha kuvunja maagano ahadi na maagizo yote ya Mungu, omba neema na rehema na msamaha kwa Mungu, badilika fanya mageuzi makubwa na rudi katika njia iliyo sahihi kwa Mungu

 

Matendo 3:18-20 “Lakini mambo yale aliyohubiri Mungu tangu zamani kwa kinywa cha manabii wake wote, ya kwamba Kristo wake atateswa, ameyatimiza hivyo. Tubuni basi, mrejee, ili dhambi zenu zifutwe, zipate kuja nyakati za kuburudishwa kwa kuwako kwake Bwana; apate kumtuma Kristo Yesu mliyewekewa tangu zamani;”

 

Warumi 12:2 “Wala msiifuatishe namna ya dunia hii; bali mgeuzwe kwa kufanywa upya nia zenu, mpate kujua hakika mapenzi ya Mungu yaliyo mema, ya kumpendeza, na ukamilifu.”

 

3.      Amini katika msamaha wa Mungu – Lazima umwendee yeye kwa imani, ukiamini katika msamaha wake, omba rehema, mweleze Mungu kile ambacho umeharibu, amini katika neno lake ambalo limesema ya kuwa tukiziungama dhambi zetu yeye atatusamehe

 

1Yohana 1:9 “Tukiziungama dhambi zetu, Yeye ni mwaminifu na wa haki hata atuondolee dhambi zetu, na kutusafisha na udhalimu wote.”

 

4.      Chukua hatua stahiki -  Kama uliondoka katika ndoa yako rudi, ulimwacha mkeo rejea kwa mkeo, ulimuacha mumeo rejea kwa mumeo, acha wanawake wote na wanaume wote ambao wanaisumbua ndoa yako, acha uasherati, acha zinaa, achana na michepuko, vunja uhusiano wako wa kimapenzi na wanawake au wanaume wote ambao wewe hujafanya nao agano, enenda katimize kile ambacho ulikuwa umekiapia au umefanya agano nacho

 

Ezra 10:1-5 “Basi hapo Ezra alipokuwa akiomba na kuungama, akilia, na kujiangusha kifudifudi mbele ya nyumba ya Mungu, wakamkusanyikia katika Israeli wote kusanyiko kubwa sana la wanaume, na wanawake, na watoto; maana watu hao walikuwa wakilia sana. Hata Shekania, mwana wa Yehieli, mmoja wa wana wa Elamu, akajibu, akamwambia Ezra, Sisi tumemkosa Mungu wetu, nasi tumeoa wanawake wageni wa watu wa nchi hizi; lakini kungaliko tumaini kwa Israeli katika jambo hili. Haya basi! Na tufanye agano na Mungu wetu, kuachana na wake zetu, na wale waliozaliwa nao, tukilifuata shauri la bwana wangu, na shauri la hao wanaoitetemekea amri ya Mungu wetu; mambo haya na yatendeke kwa kuifuata torati. Inuka; maana shughuli hii yakuhusu wewe; na sisi tu pamoja nawe; uwe na moyo mkuu, ukaitende. Ndipo Ezra akaondoka, akawaapisha wakuu wa makuhani, na Walawi, na Israeli wote, ya kwamba watafanya kama hayo. Basi wakaapa.”

 

5.      Fanya agano jipya  na Mungu – Baada ya maamuzi magumu sasa unaweza kumwambia Mungu kwa neema yako na kufanya naye agano jipya rejea kwa Mungu na dhamiria kutembea katika njia zake kama walivyofanya manabii waliotutangulia, endapo unaona yako maamuzi magumu ya kufanya tafadhali wasiliana na kiongozi wako wa kiroho, na washauri wa maswala ya kiroho kuangalia athari za maamuzi unayokwenda kuyafanya  na muongozo wake hasa kama kuna agano la kuweka sawa na kama una agano la malipizo, Kumbuka agabo linapovunjwa linadai Damu, itumie Damu ya Yesu kwa msamaha wa kweli na rehema na uwe na imani kuwa Damu hii inakunenea mema kuliko ile ya Habili.

Waebrania 12:24 “na Yesu mjumbe wa agano jipya, na damu ya kunyunyizwa, inenayo mema kuliko ile ya Habili

 

Hitimisho.

Agano wakati wote linahitaji kujitoa, unapofanya agano na Mungu ni lazima uwe umemaanisha katika hilo unalolifanya, watu wengi leo wanaingia katika maagano na kuyavunja kiwepesi kwa sababu hawatambui gharama za agano hilo, ingawa Mungu ni wa rehema nafasi ya toba bado ipo, na Mungu yuaweza kukurejeza kwake iwapo umeharibu, Mungu atawarehemu na kuwapa neema wale wote wanaojinyenyekeza na kutafuta kumrudia yeye lakini ni lazika ufanye au uchukue hatua madhubuti kujitoa katika nira zilizo kinyume na mapenzi ya Mungu naye atakuwa baba yako nawe utakuwa mwanae wa kike na wa kiume!

2Wakorintho 6:14-18 “Msifungiwe nira pamoja na wasioamini, kwa jinsi isivyo sawasawa; kwa maana pana urafiki gani kati ya haki na uasi? Tena pana shirika gani kati ya nuru na giza? Tena pana ulinganifu gani kati ya Kristo na Beliari? Au yeye aaminiye ana sehemu gani pamoja na yeye asiyeamini? Tena pana mapatano gani kati ya hekalu la Mungu na sanamu? Kwa maana sisi tu hekalu la Mungu aliye hai; kama Mungu alivyosema, ya kwamba, Nitakaa ndani yao, na kati yao nitatembea, nami nitakuwa Mungu wao, nao watakuwa watu wangu. Kwa hiyo, Tokeni kati yao, Mkatengwe nao, asema Bwana, Msiguse kitu kilicho kichafu, Nami nitawakaribisha. Nitakuwa Baba kwenu, Nanyi mtakuwa kwangu wanangu wa kiume na wa kike,”

Na. Rev. Innocent Samuel Kamote.

Mkuu wa wajenzi mwenye Hekima!