Wagalatia 6:7-8 “Msidanganyike, Mungu hadhihakiwi; kwa kuwa cho chote
apandacho mtu, ndicho atakachovuna. Maana yeye apandaye kwa mwili wake, katika
mwili wake atavuna uharibifu; bali yeye apandaye kwa Roho, katika Roho atavuna
uzima wa milele.”
Utangulizi:
Mojawapo ya maonyo yanayotolewa
na neno la Mungu upande wa agano la kale na agano jipya ni pamoja na kuionya
jamii kuhusu kudanganyika, katika ulimwengu huu tulio nao chanzo cha kila uovu
duniani kilisababishwa na udanganyifu uliofanywa na shetani kwa Mwanamke, na
kupitia udanganyifu dhambi ikaingia ulimwenguni na tangu wakati huo udanganyifu
umekuwa ni moja ya silaha kubwa sana ya shetani kuwaingiza wanadamu katika
mtego wa mateso na changamoto nyingi.
1Timotheo 2:13-14 “Kwa maana Adamu ndiye aliyeumbwa kwanza, na Hawa baadaye.
Wala Adamu hakudanganywa, ila mwanamke alidanganywa kabisa akaingia katika hali
ya kukosa.”
Ni kwaajili hiyo maandiko yana
maonyo mengi sana ambayo yanayotuonya kuhusu uwezekano wa kuingizwa kwenye
udanganyifu, leo basi tutachukua muda kujifunza maeneo kadhaa ambayo kwa hayo
maandiko yametuonya kwamba tuwe makini kwa sababu uko uwezekano wa kudanganyika
katika hayo, na kwa sababu hiyo tutaweza kuchukua tahadhari katika maisha yetu
ya kiroho, na kimwili, tutajifunza somo hili Msidanyanyike kwa kuzingatia
vipengele vitatu vifuatavyo:-
·
Maana ya
neno Msidanganyike.
·
Jinsi
mwanadamu anavyoweza kudanganyika.
·
Jinsi ya
kufanya ili kuepuka udanganyifu.
Maana ya neno Msidanganyike.
Ni muhimu kufahamu kuwa mojawapo
ya sababu kubwa ya Bwana wetu Yesu Kristo kuweka wengine katika kanisa kuwa
Mitume, Manabii, Wainjilisti, Wachungaji na Waalimu ni ili waujenge mwili wa
Kristo, hata kazi ya huduma itendeke, hata sote tukue na kufikia katika cheo
cha kimo cha utumilifu wa Kristo, lakini zaidi pia wakristo wasiwe tena
wachanga na kuchukuliwa na kila aina ya upepo wa elimu kwa kufuata njia za
udanganyifu, hii maana yake ni kuwa kanisa tusiposimama vizuri uwezekano wa
watu kudanganywa upo, uwezekano wa watu kufuata mafundisho ya uongo upo ona
Waefeso 4:11-14 “Naye alitoa wengine kuwa mitume, na wengine kuwa manabii;
na wengine kuwa wainjilisti na wengine kuwa wachungaji na waalimu; kwa kusudi
la kuwakamilisha watakatifu, hata kazi ya huduma itendeke, hata mwili wa Kristo
ujengwe; hata na sisi sote tutakapoufikia umoja wa imani na kumfahamu sana
Mwana wa Mungu, hata kuwa mtu mkamilifu, hata kufika kwenye cheo cha kimo cha
utimilifu wa Kristo; ili tusiwe tena watoto wachanga, tukitupwa huku na huku,
na kuchukuliwa na kila upepo wa elimu, kwa hila ya watu, kwa ujanja,
tukizifuata njia za udanganyifu”.
Udanganyifu hasa ni nini? Neno udanganyifu katika agano la kale
linasomeka kwa lugha ya kiebrania kama “nāshā”
na linasomeka hivyo katika agano jipya
kwa kiyunani kama neno “planáō” ambayo kwa kiingereza maana
yake hufafanuliwa kwa neno Deceivableness
ambalo maana yake ni kudanganyika au kukengeushwa “to be lead astray” au neno la kiebrania “pāthāh” kudanganywa kwa kuvutiwa “to be entice” au “to be tempted by
attract”, kujaribiwa kwa ushawishi, kwa hiyo shetani na watumishi wake
yaani manabii wa uongo, na walimu wa uongo, na mitume wa uwongo, hawatakuja
katika namna ambayo wewe utashituka kuwa huu ni uwongo, lakini watakuja katika
namna ya kushawishi, kwa kusudi la kuleta ukengeufu, shetani hatakuja katika
namna ya kutisha kwanza hatishi, kwa sababu yeye aliumbwa kama malaika, haji
kwa vitisho, lakini atakuja kama malaika wa nuru, na akitumia njia ya ushawishi.
2Wakorintho 11:13-15 “Maana watu kama hao ni mitume wa uongo, watendao kazi kwa
hila, wanaojigeuza wawe mfano wa mitume wa Kristo. Wala si ajabu. Maana Shetani
mwenyewe hujigeuza awe mfano wa malaika wa nuru. Basi si neno kubwa watumishi
wake nao wakijigeuza wawe mfano wa watumishi wa haki, ambao mwisho wao utakuwa
sawasawa na kazi zao.”
Mwanzo 3:4-6 “Nyoka akamwambia mwanamke, Hakika hamtakufa, kwa maana
Mungu anajua ya kwamba siku mtakayokula matunda ya mti huo, mtafumbuliwa macho,
nanyi mtakuwa kama Mungu, mkijua mema na mabaya. Mwanamke alipoona ya kuwa ule
mti wafaa kwa chakula, wapendeza macho, nao ni mti wa kutamanika kwa maarifa,
basi alitwaa katika matunda yake akala, akampa na mumewe, naye akala.”
Kwa hiyo kila mtu mwenye nia ya
kumtafuta Mungu kwa dhati anapaswa kuchukua tahadhari, kuhusiana na uwezekano
wa kudanganywa, kunakoratibiwa na shetani na watumishi wake, hii maana yake ni
nini wako mitume wa kweli, manabii wa kweli, wainjilishi wa kweli na wachungaji
na walimu wa kweli, na hata washirika wa kweli, lakini pia wako watumishi wa
uwongo wakiwakilisha au wakitumia majina hayo hayo, na wote sisi ni walengwa wa
kudanganywa, unaweza kudanganywa hata na mtumishi mwenzako, lakini pia unaweza
kudanganywa hata na washirika wa uwongo, kwa hiyo onyo la kuchukua tahadhari
tusidanganyike linatuhusu wote.
Jinsi mwanadamu anavyoweza kudanganyika
Yako mambo kadhaa wa kadhaa
ambayo kimsingi tusipoyatilia maanani tunaweza kujikuta kuwa tumedanganyika,
Maandiko yameorodhesha maswala kadhaa ambayo kama tutayazingatia tunaweza kuwa
salama na kama tusipoyazingatia tunaweza kujikuta kuwa tumeingia matatani na
kudanyanyika, kumbuka udanganyifu ambao shetani anaukusudia licha ya kuwalenga
wanadamu wote lakini kusudi kubwa hasa ni kuwalenga wale waliookolewa ili wote
kwa ujumla waweze kupotea, sasa tunawezaje kudanganyika hapa neno la Mungu
linaelezea namna mwanadamu anavyoweza kudanganyika:-
·
Tukisema
kwamba hatuna dhambi – Moja ya njia hatari sana anayoitumia shetani hasa
kwa watu tuliookoka ni kutuingizia mawazo ya kijinga ya kujifikiri kuwa hatuna
dhambi au tumekuwa wakamilifu, huku ni kudanganyika, haijalishi tunajitahidi
kwa kiasi gani hatuwezi kamwe kufikia ngazi ya kujitangaza kuwa tumekamilika na
hatuna dhambi, Mungu ni Mtakatifu sana na kamwe kwa utakatifu wake hakuna
mwanadamu anayeweza kufikia viwango anavyovihitaji, kila wakati unapomsogelea
Mungu utaweza kuhisi mapungufu yako na kwa sababu hiyo hakuna mwanadamu
anayeweza kukiri kuwa yeye ni mkamilifu na amemaliza ukamilifu wetu na
kuhesabiwa kwetu haki mbele za Mungu kunatokana na ukamilifu wa Yesu Kristo na
sio sisi wenyewe, wala juhudi zetu hazina mchango wowote, furaha yetu ya wokovu
tunaweza kusema ni kwa sababu tumesamehewa dhambi zetu na kuhesabiwa haki bure
kwa Imani na kwa kuzaliwa mara ya pili na kwa kutakaswa kwa damu yake Yesu, kwa
hiyo kusema kuwa hatuna dhambi ni kujidanganya
1Yohana 1: 8-10 “Tukisema kwamba hatuna dhambi,
twajidanganya wenyewe, wala kweli haimo mwetu. Tukiziungama dhambi zetu, Yeye
ni mwaminifu na wa haki hata atuondolee dhambi zetu, na kutusafisha na udhalimu
wote.Tukisema kwamba hatukutenda dhambi, twamfanya Yeye kuwa mwongo wala neno
lake halimo mwetu.”
Isaya 65:5 “watu wasemao, Simama peke yako,
usinikaribie mimi, kwa maana mimi ni mtakatifu kuliko wewe; watu hao ni moshi
puani mwangu, moto uwakao mchana kutwa.”
Tabia ya
kutokunyenyekea na kujihesabia haki inamuudhi sana Mungu, kimsingi neno la
Mungu halitutii moyo kutenda dhambi hata kidogo, lakini Mkristo wa kweli ni
yule ambaye ataendelea kujitakasa kila siku, na kuendelea kumuomba Mungu
msamaha, kila iitwapo leo, na kuendelea mbele kwa kuishi maisha matakatifu bila
ya kujikweza kwa Mungu na kujifikiri kuwa tumekamilika, Mitume walikuwa
wanyenyekevu sana hawakuwahi kujikweza na kujiweka katika kundi la watu
waliokamilika badala yake walionyesha kuwa wanaendelea kupambana, Kristo Yesu
katika mafundisho yake alionya wazi tabia ya kujifikiri kuwa umefika na kufikiri
ya kuwa tunafaa na wakati mwingine ukijilinganisha na wengine na kujijengea
tabia ya kiburi ya kujidhania kuwa wewe umekamilika haya yakijengeka ndani yetu
ni rahisi kukataliwa.
Yakobo 3:2 “Maana twajikwaa sisi sote pia katika
mambo mengi. Mtu asiyejikwaa katika kunena, huyo ni mtu mkamilifu, awezaye
kuuzuia na mwili wake wote kama kwa lijamu.”
Wafilipi 3:12-14 “Si kwamba nimekwisha kufika, au
nimekwisha kuwa mkamilifu; la! Bali nakaza mwendo ili nipate kulishika lile
ambalo kwa ajili yake nimeshikwa na Kristo Yesu. Ndugu, sijidhanii nafsi yangu
kwamba nimekwisha kushika; ila natenda neno moja tu; nikiyasahau yaliyo nyuma,
nikiyachuchumilia yaliyo mbele; nakaza mwendo, niifikilie mede ya thawabu ya
mwito mkuu wa Mungu katika Kristo Yesu.”
Luka 18:10-14 “Watu wawili walipanda kwenda
hekaluni kusali, mmoja Farisayo, wa pili mtoza ushuru. Yule Farisayo akasimama
akiomba hivi moyoni mwake; Ee Mungu, nakushukuru kwa kuwa mimi si kama watu
wengine, wanyang'anyi, wadhalimu, wazinzi, wala kama huyu mtoza ushuru. Mimi
nafunga mara mbili kwa juma; hutoa zaka katika mapato yangu yote. Lakini yule
mtoza ushuru alisimama mbali, wala hakuthubutu hata kuinua macho yake mbinguni,
bali alijipiga-piga kifua akisema, Ee Mungu, uniwie radhi mimi mwenye dhambi. Nawaambia,
huyu alishuka kwenda nyumbani kwake amehesabiwa haki kuliko yule; kwa maana
kila ajikwezaye atadhiliwa, naye ajidhiliye atakwezwa.”
Luka 6:41-42. “Basi, mbona wakitazama kibanzi
kilicho ndani ya jicho la ndugu yako, na boriti iliyo ndani ya jicho lako
mwenyewe huiangalii? Au, utawezaje kumwambia ndugu yako, Ndugu yangu, niache
nikitoe kibanzi kilicho ndani ya jicho lako, nawe huiangalii boriti iliyo ndani
ya jicho lako mwenyewe? Mnafiki wewe, itoe kwanza ile boriti katika jicho lako
mwenyewe, ndipo utakapoona vema kukitoa kile kibanzi kilichomo katika jicho la
ndugu yako.”
Mungu ndiye
anayetuhesabia haki, ni yeye ndiye aliyetufia, na ni yeye ndiye aliyetuokoa na
kutusafisha na kutuhesabia haki na ni yeye ndiye anayetuombea na ameketi mkono
wa kuume wa Mungu, kwa hiyo kila mtu aliyeokolewa anapaswa kuwa mnyenyekevu, na
kuacha kujivunia neema ya Mungu, badala yake kuipokea kwa shukurani na
unyenyekevu, na kuendelea kujitakasa kila iitwapo leo huku tukiacha kabisa
tabia ya kuwanyooshea wengine vidole, na kujihesabia haki. Endapo tutajipima
wenyewe na kujifikiri kuwa tunafaa tutakuwa tumedanganyika.
·
Tukijifikiri
kuwa tuna hekima ya dunia – Hekima ya dunia hii maana yake ni Elimu za fani
mbalimbali hapa duniani, kuwa na elimu sio jambo baya kwa sababu maandiko
yanatia moyo swala zima la kusoma, lakini tukiwa na kiburi kwa sababu ya elimu
ya dunia hii, na kupuuzia maswala ya Mungu eti kwa sababu tumesoma maandiko
yanatuambia huko ni kudanganyika, awaye yote ambaye hataki kuongozwa na neno la
Mungu ni mpuuzi bila kujali kuwa ana elimu kiasi gani, Neno la Mungu linasema
kuwa Mungu ameifanya hekima ya dunia hii kuwa ni upuuzi, kwa hiyo kujivunia
elimu ni kujidanganya, Elimu ni nyenzo ya kuturahisishia kazi na sio nyenzo ya
kutujengea kiburi dhidi ya Mungu na watu wengine.
1Wakorintho 3:18-20 “Mtu
asijidanganye mwenyewe; kama mtu akijiona kuwa mwenye hekima miongoni mwenu
katika dunia hii, na awe mpumbavu, ili apate kuwa mwenye hekima. Maana hekima
ya dunia hii ni upuzi mbele za Mungu. Kwa maana imeandikwa, Yeye ndiye
awanasaye wenye hekima katika hila yao.Na tena, Bwana anayafahamu mawazo ya
wenye hekima ya kwamba ni ya ubatili.”
·
Kama
tukiongozwa na Mapokeo ya wanadamu – mapokeo ya wanadamu ni utaratibu wa fulani
wa kijamii katika imani, ni muundo wa desturi zilizorithiwa katika kundi fulani
au dhehebu fulani na kuingizwa katika imani huku yakiwa sio msingi uliojengeka
katika neno la Mungu, mapokeo haya yamekuwa sababu ya kudanganyika kwa watu
wengi sana baadhi ya mapokeo haya ni
kama vile ubatizo kwa watu wasioamini kama watoto wachanga, kuomba kwa kutumia
Rozali, kuabudu kwa kuhusisha sanamu, pamoja na kuandama mwezi na kuutiisha
mwili kwa ukali, kutawadha na kadhalika watu
wanaofuata mapokeo hayo wamedanganyika
Wakolosai 2:4-8 “Nasema neno hili, mtu asije
akawadanganya kwa maneno ya kuwashawishi. Maana nijapokuwa sipo kwa mwili,
lakini nipo pamoja nanyi kwa roho, nikifurahi na kuuona utaratibu wenu na
uthabiti wa imani yenu katika Kristo. Basi kama mlivyompokea Kristo Yesu,
Bwana, enendeni vivyo hivyo katika yeye; wenye shina na wenye kujengwa katika
yeye; mmefanywa imara kwa imani, kama mlivyofundishwa; mkizidi kutoa shukrani.
Angalieni mtu asiwafanye mateka kwa elimu yake ya bure na madanganyo matupu,
kwa jinsi ya mapokeo ya wanadamu, kwa jinsi ya mafundisho ya awali ya
ulimwengu, wala si kwa jinsi ya Kristo.”
Mathayo 15:7-9 “Enyi wanafiki, ni vema alivyotabiri
Isaya kwa habari zenu, akisema, Watu hawa huniheshimu kwa midomo; Ila mioyo yao
iko mbali nami. Nao waniabudu bure, Wakifundisha mafundisho Yaliyo maagizo ya
wanadamu.”
·
Kufikiri
kuwa unaweza kuurithi ufalme wa Mungu huku unaendelea na maisha ya dhambi – mtu
awaye yote anayedhani ya kuwa anaweza kuurithi ufalme wa Mungu huku akiwa
anaendelea na maisha ya dhambi mtu wa namna huyo amedanganyika, mtu aliyeokoka
ni lazima aishi mbali na dhambi, lazima uache kuvuta bangi, kula madawa ya
kulevywa, kujihusisha na maswala ya utoaji wa mimba, kuuza baa, kutoa huduma za
guest house za kufanyia ngozo, kuuza pombe, kujihusisha na duluma, kuishi
maisha ya uasherati, kuabudu sanamu, kuzini, kujihusisha na ufiraji, ulawiti, ulevi, tamaa mbaya, ushoga,
usagaji, kutukana, wizi na utapeli, uchafu, mapenzi ya jinsia moja, uchawi,
ushirikina, uadui, ugomvi, wivu wenye uchungu, fitina, majungu, mafarakano,
uzushi, husuda, ulafi, picha za ngono na maswala yote yanayofanana na hayo kama
wakristo watayatenda hayo neno la Mungu liko wazi watakuwa wamedanganyika na
hawataweza kuurithi ufalme wa Mungu
1Wakorintho 6:9-10 “Au hamjui ya kuwa wadhalimu
hawataurithi ufalme wa Mungu? Msidanganyike; waasherati hawataurithi ufalme wa
Mungu, wala waabudu sanamu, wala wazinzi, wala wafiraji, wala walawiti, wala
wevi, wala watamanio, wala walevi, wala watukanaji, wala wanyang'anyi.”
Wagalatia 5:19-21 “Basi matendo ya mwili ni dhahiri,
ndiyo haya, uasherati, uchafu, ufisadi, ibada ya sanamu, uchawi, uadui, ugomvi,
wivu, hasira, fitina, faraka, uzushi, husuda, ulevi, ulafi, na mambo
yanayofanana na hayo, katika hayo nawaambia mapema, kama nilivyokwisha
kuwaambia, ya kwamba watu watendao mambo ya jinsi hiyo hawataurithi ufalme wa
Mungu.”
·
Tukiwa
wasikiaji wa neno na sio watendaji – Kusikia neno la Mungu sio kitu kibaya
kila mtu anapaswa kuwa msikivu kwa neno la Mungu lakini hiyo pekee haitoshi, ni
lazima tulitii neno la Mungu, kutii ndio kulifanyia kazi, ndio kuwa watendaji
wa neno, Mungu hakutuokoa kwaajili ya kusikia, Mungu ametuokoa kwa sababu
tumeamini, na kama tumeamini basi kila mwamini wa kweli ni yule anayelitendea
kazi neno la Mungu na kulitendea kazi kunahusisha kutii
Yakobo 1:22-25 “Lakini iweni watendaji wa neno, wala
si wasikiaji tu, hali mkijidanganya nafsi zenu. Kwa sababu mtu akiwa ni
msikiaji wa neno tu, wala si mtendaji, mtu huyo ni kama mtu anayejiangalia uso
wake katika kioo. Maana hujiangalia, kisha huenda zake, mara akasahau jinsi
alivyo. Lakini aliyeitazama sheria kamilifu iliyo ya uhuru, na kukaa humo,
asiwe msikiaji msahaulifu, bali mtendaji wa kazi, huyo atakuwa heri katika
kutenda kwake.”
Katika ufalme wa
Mungu utendaji una tmanani kubwa sana kuliko maneno na Muitikio, kimsingi
kutendea kazi neno la Mungu ni hekima na kutokulitendea kazi neno la Mungu ni
upumbavu, Bwana ampe neema kila mmoja wetu asidanganyike kwa kutokulitendea
kazi neno
Mathayo 21:28-31 “Lakini mwaonaje? Mtu mmoja alikuwa
na wana wawili; akamwendea yule wa kwanza, akasema, Mwanangu, leo nenda kafanye
kazi katika shamba la mizabibu. Akajibu akasema, Naenda, Bwana; asiende.
Akamwendea yule wa pili, akasema vile vile. Naye akajibu akasema, Sitaki;
baadaye akatubu, akaenda. Je! Katika hao wawili ni yupi aliyefanya mapenzi ya
babaye? Wakamwambia, Ni yule wa pili. Basi Yesu akawaambia, Amin nawaambia,
watoza ushuru na makahaba wanatangulia mbele yenu kuingia katika ufalme wa
Mungu.”
Mathayo 7:24-27 “Basi kila asikiaye hayo maneno
yangu, na kuyafanya, atafananishwa na mtu mwenye akili, aliyejenga nyumba yake
juu ya mwamba; mvua ikanyesha, mafuriko yakaja, pepo zikavuma, zikaipiga nyumba
ile, isianguke; kwa maana misingi yake imewekwa juu ya mwamba. Na kila asikiaye
hayo maneno yangu asiyafanye, atafananishwa na mtu mpumbavu, aliyejenga nyumba
yake juu ya mchanga; mvua ikanyesha, mafuriko yakaja, pepo zikavuma, zikaipiga
nyumba ile, ikaanguka; nalo anguko lake likawa kubwa.”
·
Kujifikiri
kuwa kitu – kujifikiri kuwa kitu mbele za Mungu ni kujidanganya, Neno
kujifikiri kuwa kitu katika lugha ya
kiyunani linatumika neno “tis” kwa
kiingereza linatumika neno “enclitic” kwa
kiyunani “enklitikos” au “enkilinesthai”
kwa lugha nyepesi “to lean on” au
“to rely on” hii ni tabia ya kufikiri kuwa mambo hayawezi kwenda bila mtu
huyo kuwepo, ni kujifikiri kuwa wewe ni maalumu sana na kuwa wewe ni wa
kutegemewa, usipokuwepo wewe mambo hayaendi, huku ndio kujiona kuwa kitu,
hii nitabia ya kiburi cha uzima, na
kiburi cha kibinadamu, mtu moja alisema hakuna mtu anayeweza kujifikiri kuwa
yeye ni wa muhimu sana na kama unafikiri kuwa wewe ni wa muhimu sana kufa na
utaona mambo yote yataenda, yataenda bila msaada wako, mkeo au mumeo ataishi,
watoto wako wataishi, wazazi wako maisha yataendelea lakini zaidi ya yote kazi
ya Mungu itaendela bila kujali wewe ni wa muhimu kiasi gani, kujiona kuwa kitu
ni dhambi na ni kiburi, dumia
imewahi kuwa na watu mashuhuri sana na wamepita na mambo yanaenda hata bila
wao, wewe na mimi sio wa kujiona kuwa kitu na kufikiri kuwa bila wewe na mimi
mambo hayatakwenda yataenda na utakachoambulia ni kupewa neno RIP tu ukizikwa
tu habari yako inaishia hapo n ahata waliokuwa wakikulilia hawalii tena.
Wagalatia 6:2-3 “Mchukuliane mizigo na kuitimiza
hivyo sheria ya Kristo. Maana mtu akijiona kuwa ni kitu, naye si kitu,
ajidanganya nafsi yake.”
·
Kupuuzia
dalili za siku za mwisho – Maandiko hayajatuelezea siku ya kurudi kwa Yesu
Kristo, lakini yametupa dalili za siku za mwisho na kurudi kwake Bwana wetu
Yesu Kristo, kupuuzia dalili tulizopewa na kuhusu kurudi kwa Bwana Yesu na
Matukio ya mwisho wa dunia ni kudanganyika, wako watu wanapuuzia swala zima la
kurudi kwa bwana wetu Yesu huku wakilichukulia swala hili kama mzaha, Kristo
Yesu alionya kuwa ni lazima tuchukue tahadhari kwa kadiri tuonavyo dalili zile
zikiwa zinakaribia, maandiko yanaonyesha kutakuwa na udanganyifu wa aina nyingi
sana kuhusiana na nyakati za mwisho na ujio wa Bwana Yesu.
Luka 21:7-8 “Wakamwuliza wakisema, Mwalimu, mambo
hayo yatakuwa lini? Nayo ni nini ishara ya kuwa mambo hayo ya karibu kutukia?
Akasema, Angalieni, msije mkadanganyika, kwa sababu wengi watakuja kwa jina
langu, wakisema, Mimi ndiye; tena, Majira yamekaribia. Basi msiwafuate hao.”
2Wathesalonike 2:3-4 “Mtu awaye yote
asiwadanganye kwa njia yo yote; maana haiji, usipokuja kwanza ule ukengeufu;
akafunuliwa yule mtu wa kuasi, mwana wa uharibifu; yule mpingamizi, ajiinuaye
nafsi yake juu ya kila kiitwacho Mungu ama kuabudiwa; hata yeye mwenyewe kuketi
katika hekalu la Mungu, akijionyesha nafsi yake kana kwamba yeye ndiye Mungu.”
·
Kupuuzia
swala la marafiki wabaya – Marafiki wabaya wanaweza kuchangia swala zima la
kudanganyika kiimani, Paulo mtume aliwaonya wakorintho kutokuwa na marafiki
wabaya “Bad company” biblia ya
Kiswahili imetumia neno mazungumzo mabaya, hawa walikuwa ni waalimu wa uwongo,
watu waliokuwa wanafundisha kuwa hakuna ufufuo wa wafu, jambo ambalo
lingepelekea kuondoa tumaini la muhimu duniani na kuwafanya watu waishi vile
wanavyotaka, au kwa anasa kwa sababu ya kutckuwa na matumaini, kimsingi
maandiko yanatuonya kutokuwa na ufungamanifu wa ndani sana na watu ambao
wanaonekana kuwa na imani potofu au iliyo kinyume na yetu au ile misingi
uliyojifunza, kwani kwa kuruhusu hayo tunaweza kudanganyika na kupokea
ukengeufu, udanganyifu.
1Wakorintho 15:32-34 “Ikiwa, kwa
jinsi ya kibinadamu, nalipigana na hayawani wakali kule Efeso, nina faida gani?
Wasipofufuliwa wafu, na tule, na tunywe, maana kesho tutakufa. Msidanganyike;
Mazungumzo mabaya huharibu tabia njema.Tumieni akili kama ipasavyo, wala
msitende dhambi; kwa maana wengine hawamjui Mungu. Ninanena hayo niwafedheheshe.”
2Wakorintho 6:14-18 “Msifungiwe nira
pamoja na wasioamini, kwa jinsi isivyo sawasawa; kwa maana pana urafiki gani
kati ya haki na uasi? Tena pana shirika gani kati ya nuru na giza? Tena pana
ulinganifu gani kati ya Kristo na Beliari? Au yeye aaminiye ana sehemu gani
pamoja na yeye asiyeamini? Tena pana mapatano gani kati ya hekalu la Mungu na
sanamu? Kwa maana sisi tu hekalu la Mungu aliye hai; kama Mungu alivyosema, ya
kwamba, Nitakaa ndani yao, na kati yao nitatembea, nami nitakuwa Mungu wao, nao
watakuwa watu wangu. Kwa hiyo, Tokeni kati yao, Mkatengwe nao, asema Bwana,
Msiguse kitu kilicho kichafu, Nami nitawakaribisha. Nitakuwa Baba kwenu, Nanyi
mtakuwa kwangu wanangu wa kiume na wa kike,”
·
Kuzungumza
maneno yasiyo na maana ya uasi – Uasi ni sumu inayoenea kwa haraka sana,
neno la Mungu linatuelekeza kuwa kufuata maneno ya kuasi yasiyo na maana ni kudanganyika, maandiko
yanatutaka wakati wote tuzungumze maneno yenye kujenga na wala sio ya kubomoa,
wala hatupaswi kufuata mkumbo wa wale wanaoasi ili tuweze kuwa salama,
kuchochea kwa gharama yoyote ile maneno ya uasi kunatuweka katika nafasi ya
kudanganyika na kuruhusu hasira ya Mungu kuja juu yetu
Waefeso 5:6-11 “Mtu asiwadanganye kwa maneno yasiyo
na maana; kwa kuwa kwa sababu ya hayo hasira ya Mungu huwajia wana wa uasi.
Basi msishirikiane nao. Kwa maana zamani ninyi mlikuwa giza, bali sasa mmekuwa
nuru katika Bwana; enendeni kama watoto wa nuru, kwa kuwa tunda la nuru ni
katika wema wote na haki na kweli; mkihakiki ni nini impendezayo Bwana. Wala
msishirikiane na matendo yasiyozaa ya giza, bali myakemee;”
Mathayo 12:34-37 “Enyi wazao wa nyoka, mwawezaje
kunena mema, mkiwa wabaya? Maana, kinywa cha mtu huyanena yaujazayo moyo wake.
Mtu mwema katika akiba njema hutoa mema; na mtu mbaya katika akiba mbaya hutoa
mabaya. Basi, nawaambia, Kila neno lisilo maana, watakalolinena wanadamu,
watatoa hesabu ya neno hilo siku ya hukumu. Kwa kuwa kwa maneno yako
utahesabiwa haki, na kwa maneno yako utahukumiwa.”
·
Kujivunia
Dini au dhehebu kuliko utakatifu – Maandiko yanaonyesha wazi kuwa kujivunia
dini kuliko maisha matakatifu ni aina nyingine ya udanganyifu, nyakati za leo
watu husifia dini zao na madhehebu yao na wameacha kabisa kumuinua Kristo kwa
maneno yao na kwa matendo yao, Nyakati za kanisa la kwanza watu walijivunia
dini, huku Yatima na wajane wakiishi katika wakati mgumu, hakukuwa na watu wa
kuwatunza, na hali ya kipato ilikuwa mbaya na dini zilikuwepo, badala ya watu
kuonyesha upendo kivitendo kwa kushughulika na kujali masikini na wenye
mahitaji ya kijamii, wao walijikita katika kutangaza dini zao na madhehebu yao
huku wakijisifia kuwa ni madhehebu bora, Yakobo aliwafundisha kurudi katika
upendo wa kweli kujali, jamii yenye uhitaji na kuishi maisha safi yasiyo na
taka na kutokuifuata dunia hii, kama tutajisifia kuwa tuna madehebu mazuri na dini
nzuri, huku kanisa letu likiwa limejaa ubinafsi na kutokujali, na huku watu
wake hawana upendo yaani hawajali hayo yote yatakuwa ni kazi bure na ni
kujidanganya
Yakobo 1:26-27 “Mtu
akidhani ya kuwa anayo dini, wala hauzuii ulimi wake kwa hatamu, hali akijidanganya
moyo wake, dini yake mtu huyo haifai. Dini iliyo safi, isiyo na taka mbele za
Mungu Baba ni hii, Kwenda kuwatazama yatima na wajane katika dhiki yao, na
kujilinda na dunia pasipo mawaa.”
1Wakorintho 13:1-7 “Nijaposema kwa lugha za
wanadamu na za malaika, kama sina upendo, nimekuwa shaba iliayo na upatu
uvumao.Tena nijapokuwa na unabii, na kujua siri zote na maarifa yote,
nijapokuwa na imani timilifu kiasi cha kuweza kuhamisha milima, kama sina
upendo, si kitu mimi.Tena nikitoa mali zangu zote kuwalisha maskini, tena
nikijitoa mwili wangu niungue moto, kama sina upendo, hainifaidii kitu. Upendo
huvumilia, hufadhili; upendo hauhusudu; upendo hautakabari; haujivuni; haukosi
kuwa na adabu; hautafuti mambo yake; hauoni uchungu; hauhesabu mabaya; haufurahii
udhalimu, bali hufurahi pamoja na kweli; huvumilia yote; huamini yote;
hutumaini yote; hustahimili yote.”
·
Kuufuta
moyo kuliko neno la Mungu – aina nyingine ya kudanyanyika ni ile tabia ya
kuutii moyo kuliko neno la Mungu, wako watu duniani ambao huujali sana moyo
kuliko kanuni na taratibu za kutusaidia zilizoko katika neno la Mungu, wanasema
upe moyo kitu unapenda, huku ni kuufuata mwili na ni kutaka kufa, maandiko
yanaonya kuwa kuufuata moyo ni kufuata kifo kwa sababu moyo una ugonjwa wa
kuua, Kwa hiyo ukitii kila kitu ambacho moyo unakuongoza unajikuta umeingia
pabaya na kwa kweli utakuwa umedanganyika, moyo ni chombo cha tamaa ambacho
mara nyingi huwaongoza watu wa dunia hii na sio wana wa Mungu hatuna budi
kumuomba Mungu aweke sheria zake katika mioyo yetu tusiifuate tamaa na
kudanganyika kwa sababu tamaa hukaa moyoni
Yeremia 17:9-10 “Moyo huwa mdanganyifu kuliko vitu
vyote, una ugonjwa wa kufisha; nani awezaye kuujua? Mimi, Bwana, nauchunguza
moyo, navijaribu viuno, hata kumpa kila mtu kiasi cha njia zake, kiasi cha
matunda ya matendo yake.”
Tito 3:3-5 “Maana
hapo zamani sisi nasi tulikuwa hatuna akili, tulikuwa waasi, tumedanganywa,
huku tukitumikia tamaa na anasa za namna nyingi, tukiishi katika uovu na
husuda, tukichukiza na kuchukiana. Lakini wema wake Mwokozi wetu Mungu, na
upendo wake kwa wanadamu, ulipofunuliwa, alituokoa; si kwa sababu ya matendo ya
haki tuliyoyatenda sisi; bali kwa rehema yake, kwa kuoshwa kwa kuzaliwa kwa
pili na kufanywa upya na Roho Mtakatifu;”
Yakobo 1:13-15 “Mtu ajaribiwapo, asiseme,
Ninajaribiwa na Mungu; maana Mungu hawezi kujaribiwa na maovu, wala yeye
mwenyewe hamjaribu mtu. Lakini kila mmoja hujaribiwa na tamaa yake mwenyewe
huku akivutwa na kudanganywa.Halafu ile tamaa ikiisha kuchukua mimba huzaa dhambi,
na ile dhambi ikiisha kukomaa huzaa mauti.”
Jambo kubwa na
la msingi ni kuujaza moyo wetu kwa neno la Mungu ili lituongoze lenyewe ndani
ya moyo wetu badala ya kuufuata moyo, bila neno la Mungu moyo utatuendesha sawa
na kawaida ya ulimwengu huu, Mwandishi wa Zaburi anaonyesha jinsi alivyoliweka
neno la Mungu moyoni mwake na kumuomba Mungu asiongozwe na moyo kusudi kubwa ni
ili asimtende Mungu dhambi.
Zaburi 119:9-11 “Jinsi gani kijana aisafishe njia
yake? Kwa kutii, akilifuata neno lako. Kwa moyo wangu wote nimekutafuta,
Usiniache nipotee mbali na maagizo yako. Moyoni mwangu nimeliweka neno lako,
Nisije nikakutenda dhambi.”
·
Kupenda
kutiwa moyo kuliko kukemewa na Bwana – Ni muhimu kufahamu kuwa ni rahisi
sana kudanganyika pale watu wanapotutia moyo zaidi kuliko kutukemea, mojawapo
ya kazi za kinabii ni pamoja na kutia moyo na kukemea, Neno la Mungu limeweka
wazi kuwa Mwana yule anayependwa na baba yake hukemewa, na ikiwa hakuna
kukemewa basi unakuwa mwana wa haramu
Waebrania 12:5-8 “tena mmeyasahau yale maonyo,
yasemayo nanyi kama kusema na wana, Mwanangu, usiyadharau marudia ya Bwana,
Wala usizimie moyo ukikemewa naye; Maana yeye ambaye Bwana ampenda, humrudi,
Naye humpiga kila mwana amkubaliye. Ni kwa ajili ya kurudiwa mwastahimili;
Mungu awatendea kama wana; maana ni mwana yupi asiyerudiwa na babaye? Basi kama
mkiwa hamna kurudiwa, ambako ni fungu la wote, ndipo mmekuwa wana wa haramu
ninyi, wala si wana wa halali.”
Nyakati za
biblia kama ilivyo nyakati za leo watu wengi wakiwemo wafalme hawakuwa wanafurahia
sana kukemewa, na badala yake wengi walipenda kutiwa moyo na kuambiwa kila
wakati Amani, Amani Amani, jambo hili lilimuudhi sana Mungu na hivyo Mungu
aliwaachia manabii wa uwongo wawadanganye, hawa ni manabii ambao kimsingi Mungu
hakuwatuma lakini walijikinai wakijua mioyo ya watu inataka nini na wakafanya
kama watakavyo na kuwatabiria mema, tu kumbe pepo wa uongo walikuwa wamechukua
nafasi ya kuwadanganya
Yeremia 29:8-9 “Maana Bwana wa majeshi, Mungu wa
Israeli, asema hivi, Manabii walio kati yenu, na wabashiri wenu, wasiwadanganye
ninyi, wala msisikilize ndoto zenu, mnazootesha. Kwa maana kwa jina langu
hutabiri maneno ya uongo kwenu; mimi sikuwatuma, asema Bwana.”
Yeremia 23:25-28 “Nimesikia waliyoyasema manabii
wanaotabiri uongo kwa jina langu, wakisema, Nimeota ndoto; nimeota ndoto. Je!
Mambo hayo yatakuwa katika mioyo ya manabii wanaotabiri uongo hata lini,
manabii hao wenye udanganyifu katika mioyo yao wenyewe? Wanaodhania ya kuwa
watawasahaulisha watu wangu jina langu kwa ndoto zao, wanazomhadithia kila mtu
jirani yake, kama vile baba zao walivyolisahau jina langu, kwa ajili ya Baali.
Nabii aliye na ndoto, na aseme ndoto yake; na yeye aliye na neno langu, na
aseme neno langu kwa uaminifu. Makapi ni kitu gani kuliko ngano? Asema Bwana.”
1Wafalme 22:2-23 “Ikawa, mwaka wa tatu Yehoshafati
mfalme Wa Yuda akamshukia mfalme wa Israeli. Mfalme wa Israeli akawaambia
watumishi wake, Je! Hamjui ya kuwa Ramoth-Gileadi ni yetu? Nasi tumenyamaza
tusiitwae mkononi mwa mfalme wa Shamu? Akamwambia Yehoshafati, Je! Utakwenda
nami tupigane na Ramoth-gileadi? Yehoshafati akamwambia mfalme wa Israeli, Mimi
ni kama wewe, na watu wangu ni kama watu wako na farasi zangu ni kama farasi
zako.Yehoshafati akamwambia mfalme wa Israeli, Uulize leo, nakusihi, kwa neno
la Bwana. Ndipo mfalme wa Israeli akawakusanya pamoja manabii, kama watu mia
nne. Akawaambia Je! Niende juu ya Ramoth-Gileadi kuupiga vita, au ninyamaze?
Wakasema Kwea; kwa kuwa Bwana atautia mkononi mwa mfalme. Lakini Yehoshafati
akasema, Je! Hayupo hapa nabii wa Bwana tena, ili tumwulize yeye? Mfalme wa
Israeli akamwambia Yehoshafati, Yupo mtu mmoja, ambaye tungeweza kumwuliza
Bwana kwa yeye, yaani Mikaya mwana wa Imla; lakini namchukia; kwa sababu
hanibashirii mema, ila mabaya. Yehoshafati akasema, La! Mfalme asiseme hivi.
Ndipo mfalme wa Israeli akamwita akida, akamwambia, mlete hima Mikaya mwana wa
Imla. Basi mfalme wa Israeli na Yehoshafati mfalme wa Yuda walikuwa wakikaa
kila mtu katika kiti chake cha enzi, wamevaa mavazi yao, katika sakafu langoni
pa Samaria; na manabii wote wakafanya unabii mbele yao. Na Zedekia mwana wa
Kenaana akajifanyia pembe za chuma, akasema, Bwana asema hivi, Kwa hizo
utawasukuma Washami, hata waharibike. Na manabii wote wakasema hivyo kwa
unabii, wakisema, Kwea Ramoth-Gileadi, ukafanikiwe; kwa kuwa Bwana atautia
mkononi mwa mfalme. Na yule mjumbe, aliyekwenda kumwita Mikaya, akamwambia,
akasema, Angalia sasa, maneno ya manabii kwa kinywa kimoja husema mema kwa
mfalme; neno lako na liwe, nakusihi, kama neno la mmojawapo wao, ukaseme mema.
Mikaya akasema, Kama Bwana aishivyo, neno lile Bwana aniambialo, ndilo
nitakalolinena. Na alipokuja kwa mfalme, mfalme alimwambia, Je! Mikaya, tuende
Ramoth-Gileadi kupiga vita, au tunyamaze? Akamwambia, Kwea, ufanikiwe; kwa kuwa
Bwana atautia mkononi mwa mfalme. Mfalme akamwambia, Mara ngapi nikuapishe
usiniambie neno ila yaliyo kweli, kwa jina la Bwana? Akasema, Naliwaona
Waisraeli wote wametawanyika milimani, kama kondoo wasio na mchungaji. Bwana
akasema, Hawa hawana bwana; na warudi kila mtu nyumbani kwake kwa amani. Mfalme
wa Israeli akamwambia Yehoshafati, Je! Sikukuambia, hatanibashiria mema, ila
mabaya? Mikaya akasema, Sikia basi neno la Bwana; Nalimwona Bwana ameketi
katika kiti chake cha enzi, na jeshi lote la mbinguni wamesimama upande wa
mkono wake wa kuume na wa kushoto. Bwana akasema, Ni nani atakayemdanganya
Ahabu, ili akwee Ramoth-Gileadi akaanguke? Basi huyu akasema hivi; na huyu
hivi. Akatoka pepo, akasimama mbele za Bwana, akasema, Mimi nitamdanganya.
Bwana akamwambia, Jinsi gani? Akasema, Nitaondoka, na kuwa pepo wa uongo
kinywani mwa manabii wake wote. Akasema, Utamdanganya, na kudiriki pia; ondoka
ukafanye hivyo. Basi angalia, Bwana ametia pepo wa uongo kinywani mwa manabii
wako hawa wote; naye Bwana amenena mabaya juu yako.”
Unaona Mungu ni
baba yetu mwenye upendo, sio kila wakati atatutia moyo tu, kuna wakati
atatukemea na kutukaripia ili kutuchonga tuweze kukamilika kwaajili ya utukufu
wake, kwa hiyo kila mtu aliyeokolewa anapaswa kukubali makemeo, makemeo hutupeleka
katika ngazi nyingine, na hutusaidia kujiangalia na kujiona kama tuko sawa na
kama hatuko sawa ni lazima tukubali kutubu, ikiwa hatutakuwa tunapenda kukemewa
Mungu ataruhusu manabii wa uongo watudanganye na kwa sababu hiyo ni rahisi
kujikuta tumepotea kumbuka wakati wote lililotukuka kwa wanadamu ni chukizo kwa
Mungu, tusidanganyike na kusifiwa na wanadamu wakati wote na badala yake
tukubali pia na kukosolewa badala ya kujaa sifa tu.
Luka 6:26 “Ole wenu ninyi watu wote
watakapowasifu, kwa kuwa baba zao waliwatenda manabii wa uongo mambo kama
hayo.Lakini nawaambia ninyi mnaosikia, Wapendeni adui zenu, watendeeni mema
wale ambao wawachukia ninyi, wabarikieni wale ambao wawalaani ninyi, waombeeni
wale ambao wawaonea ninyi.”
Luka 16:15 “Akawaambia, Ninyi ndinyi mnaojidai
haki mbele ya wanadamu, lakini Mungu awajua mioyo yenu; kwa kuwa lililotukuka
kwa wanadamu huwa chukizo mbele za Mungu.”
·
Kuamini
kuwa miujiza ilikoma – iko dhana ya baadhi ya jamii za kikristo ambao
hawaamini kuwepo kwa miujiza na uponyaji, na wanaamini katika kukoma kwa karama
za rohoni baada ya mitume na maandiko wanayoyatumia ni
1Wakorintho 13:8-13 “Upendo
haupungui neno wakati wo wote; bali ukiwapo unabii utabatilika; zikiwapo lugha,
zitakoma; yakiwapo maarifa, yatabatilika. Kwa maana tunafahamu kwa sehemu; na
tunafanya unabii kwa sehemu; lakini ijapo ile iliyo kamili, iliyo kwa sehemu
itabatilika. Nilipokuwa mtoto mchanga, nalisema kama mtoto mchanga, nalifahamu
kama mtoto mchanga, nalifikiri kama mtoto mchanga; tokea hapo nilipokuwa mtu mzima,
nimeyabatilisha mambo ya kitoto. Maana wakati wa sasa tunaona kwa kioo kwa
jinsi ya fumbo; wakati ule tutaona uso kwa uso; wakati wa sasa nafahamu kwa
sehemu; wakati ule nitajua sana kama mimi nami ninavyojuliwa sana. Basi, sasa
inadumu imani, tumaini, upendo, haya matatu; na katika hayo lililo kuu ni
upendo.”
Kuwa na imani ya
namna hiyo kwa tafasiri hii mbaya ya kimaandiko ni kudanganyika hakuna mahali
popote pale katika maandiko ambapo inathibitishwa kwa vinywa vya mashahidi
wawili au watatu kuwa miujiza, ishara na uponyaji ulikoma wakati wa mitume,
Mungu hajaacha kuwatendea mema watu wake na kama wako wanaoamini hivyo basi
wamepotoka
Yakobo 1: 16-17 “Ndugu zangu
wapenzi, msidanganyike. Kila kutoa kuliko kwema, na kila kitolewacho kilicho
kamili, hutoka juu, hushuka kwa Baba wa mianga; kwake hakuna kubadilika, wala
kivuli cha kugeuka-geuka.”
Dhana ya kwamba
ishara na miujiza na karama za utendaji wa Roho Mtakatifu kukoma havijawahi
kuthibitishwa kokote katika maandiko, Neno la Mungu linaonyesha wazi kuwa
miujiza, uponyaji na karama za Rohoni ni utendaji wa Mungu na ni sehemu ya kazi
ya Mungu kupitia kanisa lake hata leo, maandiko yanaonyesha kuwepo kwa ishara
na miujiza na karama za Roho Mtakatifu kwanza ikiwa ni pamoja na ahadi ya Yesu
Kristo mwenyewe
Yohana 14:12 “Amin, amin, nawaambieni, Yeye
aniaminiye mimi, kazi nizifanyazo mimi, yeye naye atazifanya; naam, na kubwa
kuliko hizo atafanya, kwa kuwa mimi naenda kwa Baba.”
Kukanusha kuwa
hakuna ishara na miujiza na karama za Roho Mtakatifu ni sawa tu na kukanusha au
kukataa kazi za Roho Mtakatifu, karama hizi ni zawadi zinazotolewa na Roho
Mtakatifu kwa kanisa, naelewa kuwa zinatenda kazi kwa kadiri ya viwango vya
Imani, lakini haimaanishi kuwa hakuna uponyaji huu wa kiungu.
1Wakorintho 12:4-11 “Basi pana
tofauti za karama; bali Roho ni yeye yule.Tena pana tofauti za huduma, na Bwana
ni yeye yule. Kisha pana tofauti za kutenda kazi, bali Mungu ni yeye yule
azitendaye kazi zote katika wote. Lakini kila mmoja hupewa ufunuo wa Roho kwa
kufaidiana. Maana mtu mmoja kwa Roho apewa neno la hekima; na mwingine neno la
maarifa, apendavyo Roho yeye yule; mwingine imani katika Roho yeye yule; na
mwingine karama za kuponya katika Roho yule mmoja; na mwingine matendo ya
miujiza; na mwingine unabii; na mwingine kupambanua roho; mwingine aina za
lugha; na mwingine tafsiri za lugha; lakini kazi hizi zote huzitenda Roho huyo
mmoja, yeye yule, akimgawia kila mtu peke yake kama apendavyo yeye.”
Maandiko aidha
yanaonyesha ushahidi kuwa sio mitume peke yao waliofanya miujiza na kwa sababu
hiyo awaye yote ambaye anadai kuwa karama zilikoma mara baada ya mitume hana
uwezo wa kutosha kuwa Mwalimu wa neno la Mungu, maandiko yana ushahidi wa
kutosha kuwa waamini wengine wasiokuwa mitume walitumiwa na Mungu kwa karama mbali
mbali kama ilivyokuwa kwa kanisa la korintho na mengineyo
Matendo 6:8 “Na Stefano, akijaa neema na uwezo,
alikuwa akifanya maajabu na ishara kubwa katika watu.”
Matendo 8:5-7 “Filipo akatelemka akaingia mji wa
Samaria, akawahubiri Kristo. Na makutano kwa nia moja wakasikiliza maneno yale
yaliyosemwa na Filipo walipoyasikia na kuziona ishara alizokuwa akizifanya. Kwa
maana pepo wachafu wakawatoka wengi waliopagawa nao, wakilia kwa sauti kuu; na
watu wengi waliopooza, na viwete, wakaponywa.”
Hao wanaotajwa
katika maandiko hapo juu hawakuwa mitume, lakini walitumiwa kwa viwango vikubwa
Mungu Roho Mtakatifu akifanya kazi pamoja nao bila kubagua kiviwango, wale
wanaoamini katika kifungu kile cha 1Wakorintho 13:8-13
1Wakorintho 13:8-13 “Upendo haupungui
neno wakati wo wote; bali ukiwapo unabii utabatilika; zikiwapo lugha, zitakoma;
yakiwapo maarifa, yatabatilika. Kwa maana tunafahamu kwa sehemu; na tunafanya
unabii kwa sehemu; lakini ijapo ile iliyo kamili, iliyo kwa sehemu itabatilika.
Nilipokuwa mtoto mchanga, nalisema kama mtoto mchanga, nalifahamu kama mtoto
mchanga, nalifikiri kama mtoto mchanga; tokea hapo nilipokuwa mtu mzima,
nimeyabatilisha mambo ya kitoto. Maana wakati wa sasa tunaona kwa kioo kwa
jinsi ya fumbo; wakati ule tutaona uso kwa uso; wakati wa sasa nafahamu kwa
sehemu; wakati ule nitajua sana kama mimi nami ninavyojuliwa sana. Basi, sasa
inadumu imani, tumaini, upendo, haya matatu; na katika hayo lililo kuu ni
upendo.”
Kifungu hiki
hakizungumzii hata kidogo kukoma kwa karama katika wakati huu wa sasa, Paulo
anachozungumzia hapa ni kuwa karama zitakoma wakati wa utimilifu wa wakati na huu ni ule
wakati Yesu Kristo atakaporudi na wakati wa ufalme wa mbinguni na sio
kwa wakati wa mitume wala wakati wa sasa
Aidha katika
kanisa leo ziko shuhuda mbalimbali nyingi sana za kazi za uponyaji na ishara na
miujiza inayoshuhudia kuendelea kuwepo kwa Kazi za Roho Mtakatifu, shuhuda hizi
haziwezi kupuuzwa kwa sababu nyingi zinatoka kwa watu waaminifu nikiwemo mimi
mwenyewe ambaye nimeombea watu na kuona wakiponywa, Ishara na miujiza ni sehemu
muhimu sana inayorahisisha kazi ya injili na kwa sababu hiyo Paulo mtume
aliwasihi wakorintho kutamani sana karama za rohoni, hivyo kuamini kuwa miujiza ilikoma ni imani
ya kijinga na ya kipuuzi inayotaka kupuuzia utendaji wa Roho Mtakatifu na
kulifanya kanisa kuwa taasisi ya kawaida kama ya kimwili tu isiyo na
madhihirisho ya nguvu za Mungu.
1Wakorintho 14:1 “Ufuateni upendo, na kutaka sana
karama za rohoni, lakini zaidi kwamba mpate kuhutubu.”
·
Kutokupuuzia
kanuni ya kupanda na kuvuna – Iko kanuni ambayo inatisha sana ni kanuni ya
kupanda na kuvuna wahindi wanaiita Karma, kwamba ni tambia ya kujirudia rudia
kwa matendo unayotenda, iwapo unatenda mema kuna namna utakuja kuyavuna kwa
wakati wake, lakini vile vile ukitenda yasiyopasa uko uwezekano wa kuyavuna
pia, maandiko yanatuonya kutokudanganyika katika hilo, yaani kufikiri hutavuna
kile unachokipanda kwa hiyo ukipanda katika mwili utavuna uharibifu na ukipanda
katika roho utavuna uzima milele.
Wgalatia 6:9-10 “Tena tusichoke katika kutenda mema;
maana tutavuna kwa wakati wake, tusipozimia roho. Kwa hiyo kadiri tupatavyo
nafasi na tuwatendee watu wote mema; na hasa jamaa ya waaminio.”
Wagalatia 6:7-8 “Msidanganyike, Mungu hadhihakiwi;
kwa kuwa cho chote apandacho mtu, ndicho atakachovuna. Maana yeye apandaye kwa
mwili wake, katika mwili wake atavuna uharibifu; bali yeye apandaye kwa Roho,
katika Roho atavuna uzima wa milele.”
Kama hutaki
kujiumiza moyo wako basi ni muhimu sana ukaizingatia kanuni hii, hii ni kanuni
ya ulimwengu wa roho, Mungu hulipa kisasi na kisasi ni juu yake kwa msingi huo
ni muhimu sana kujiepusha kuwafanyia watu mambo yale ambayo wewe hungependa
kufanyiwa vinginevyo uwezekano wa kanuni hii kutenda kazi unaweza kuwa mkubwa
Mathayo 7:12 “Basi yo yote myatakayo mtendewe na
watu, nanyi watendeeni vivyo hivyo; maana hiyo ndiyo torati na manabii.”
Jinsi ya kufanya ili kuepuka udanganyifu.
Maandiko yanatupa tahadhari
kwamba tuwe waangalifu ili tusije tukadanganyika kwa msingi huo yale
yaliyoelezwa katika kipengele cha pili na mengineyo ambayo sijayaorodhesha
lakini Roho wa Mungu yu aweza kukufunulia katika maandiko basi yazingatiwe ili
tusiingie katika udanganyifu.
Waebrania 3:12-19 “Angalieni, ndugu zangu, usiwe katika mmoja wenu moyo mbovu
wa kutokuamini, kwa kujitenga na Mungu aliye hai.Lakini mwonyane kila siku,
maadamu iitwapo leo; ili mmoja wenu asifanywe mgumu kwa udanganyifu wa dhambi.
Kwa maana tumekuwa washirika wa Kristo, kama tukishikamana na mwanzo wa
uthabiti wetu kwa nguvu mpaka mwisho; hapo inenwapo, Leo, kama mtaisikia sauti
yake, Msifanye migumu mioyo yenu, Kama wakati wa kukasirisha. Maana ni akina
nani waliokasirisha, waliposikia? Si wale wote waliotoka Misri wakiongozwa na
Musa? Tena ni akina nani aliochukizwa nao miaka arobaini? Si wale waliokosa,
ambao mizoga yao ilianguka katika jangwa? Tena ni akina nani aliowaapia ya
kwamba hawataingia katika raha yake, ila wale walioasi? Basi twaona ya kuwa
hawakuweza kuingia kwa sababu ya kutokuamini kwao.”
Luka 21:8 “Akasema, Angalieni, msije mkadanganyika, kwa sababu wengi
watakuja kwa jina langu, wakisema, Mimi ndiye; tena, Majira yamekaribia. Basi
msiwafuate hao.”
Na Rev. Innocent Samuel Kamote
Mkuu wa wajenzi mwenye hekima