Jumapili, 13 Julai 2025

Asizimie moyo mtu!


1Samuel 17:32-36 “Daudi akamwambia Sauli, Asizimie moyo mtu ye yote kwa ajili ya huyu; mimi mtumishi wako nitakwenda kupigana na Mfilisti huyu. Sauli akamwambia Daudi, Huwezi wewe kumwendea Mfilisti huyu upigane naye; maana wewe u kijana tu; na huyu ni mtu wa vita tangu ujana wake. Daudi akamwambia Sauli, Mtumishi wako alikuwa akichunga kondoo za baba yake, na alipokuwa akija simba, au dubu, akamkamata mwana-kondoo wa lile kundi, mimi hutoka nikamfuata, nikampiga, nikampokonya kinywani mwake; na akinirukia, humshika ndevu zake, nikampiga, nikamwua. Mtumishi wako alimwua simba na dubu pia; na huyu Mfilisti asiyetahiriwa atakuwa kama mmoja wao, kwa sababu amewatukana majeshi ya Mungu aliye hai.”


Utangulizi:

Ni muhimu kufahamu kuwa katika maisha haya mara nyingi mimi na wewe kama wanadamu huwa tunakutana na changamoto mbali mbali ambazo nyinginezo zinaweza kutuvunja moyo na kutukatisha tamaa, sio hivyo tu pia zinaweza kutuogopesha na kutufanya tupoteze kujiamini au hata kuamini kuwa Mungu anaweza kutusaidia tena, Katika Israel wakati fulani waliwahi kukutana na hali kama hii unayoipitia wewe, walikuwa katika vita na wafilisti, na katika jeshi la wafilisti alijitokeza mtu mmoja mkubwa sana mwenye nguvu na mwenye kutisha ambaye alizungumza maneno ya propaganda za kivita na kuwatia hofu sana wana wa Israel kiasi ambacho jeshi lote la Israel wakiongozwa na Sauli mfalme wao waliogopa na kuzimia moyo, Neno “Asizimie” katika Lugha ya kiebrania linasomeka kama “Nรขphal” ambalo kwa kiingereza ni “fall” limetumika hivyo mara 318 likimaanisha kuanguka, au kupoteza matumaini, au kushuka chini kutoka katika hali yake ya awali, kwa Kiswahili kuvunjika moyo yaani asivunjike moyo mtu awaye yote  unapokutana na changamoto.

1Samuel 17:1-11 “Wakati huo Wafilisti walikusanya majeshi yao kwa vita, nao wakakusanyika huko Soko, ulio mji wa Yuda, wakatua kati ya Soko na Azeka, katika Efes-damimu. Naye Sauli na watu wa Israeli wakakusanyika, wakatua katika bonde la Ela, nao wakapanga vita juu ya hao Wafilisti. Wafilisti wakasimama juu ya mlima upande huu, na Waisraeli wakasimama juu ya mlima upande huu, napo palikuwa na hilo bonde katikati. Ndipo akatoka shujaa katika kambi ya Wafilisti, aliyeitwa Goliathi, wa Gathi, ambaye urefu wake ulikuwa mikono sita na shibiri moja. Alikuwa na chapeo ya shaba kichwani, tena amevaa darii ya shaba; na uzani wake ile darii ya shaba ulikuwa shekeli elfu tano za shaba. Tena amevaa mabamba ya shaba miguuni mwake, naye alikuwa na mkuki wa shaba kati ya mabega; yake. Na mti wa fumo lake ulikuwa kama mti wa mfumaji; na kichwa cha mkuki wake kilikuwa shekeli mia sita za chuma uzito wake; na mtu aliyemchukulia ngao yake akamtangulia. Naye akasimama, akawapigia kelele majeshi ya Israeli akawaambia, Mbona mmetoka kupanga vita? Je! Mimi si Mfilisti, na ninyi si watumishi wa Sauli? Jichagulieni mtu, akanishukie mimi. Kama akiweza kupigana nami na kuniua, sisi tutakuwa watumwa wenu; nami nikimshinda yeye na kumwua, ninyi mtakuwa watumwa wetu, na kututumikia. Yule Mfilisti akasema, Nayatukana leo majeshi ya Israeli; nipeni mtu tupigane. Basi Sauli na Israeli wote waliposikia maneno hayo ya Mfilisti, wakafadhaika na kuogopa sana.”

Kutokana na maneno ya shujaa huyo wa wafilisti mwenye kutisha sana Israel waliogopa na kuzimia moyo, ni jambo la kawaida wakati mwingine kwamba linapotokea jambo la kutisha kutokana na propaganda za kishetani huwa tunasahau uweza wa Mungu na ukuu wake na kuitazama ile changamoto huku tukijiuliza kama tunaweza kutokaje katika changamoto hiyo, unajiuliza nitatoboa kweli au safari hii ndio nafariki, nitatokaje katika ugonjwa huu, nawezaje kukabiliana na deni hili kubwa namna hii, aibu inakaribia, nawezaje kutoka katika matatizo haya na kwa sababu ya utisho wa hali inayotuzunguka ni rahisi kwetu kuvunjika moyo au kuzimia moyo, Kijana mdogo sana katika Israel Daudi alisimama kwa ujasiri na kuwatia moyo taifa zima ya kuwa asizimie moyo mtu! Kwani yeye atapambana na hali inayowakabili kwa jina la Mungu wa Israel!. Leo kila changamoto unayokabiliana nayo, kila ukuta unaosimama kama kikwazo katika maisha yako, kila mlima na jaribu, na mateso, na ugonjwa na majini na mapepo na nguvu za giza zinazosimama kama changamoto katika maisha yako ambazo zimekufanya ukazimia moyo kwa jina la Yesu Kristo mwana wa Mungu aliye hai tunakwenda kukabiliana nazo na kuzisambaratisha kabisa haleluyaa Asizimie moyo mtu!.Tutajifunza somo hili Asizimie Moyo mtu kwa kuzuingatia vipengele vitatu vifuatavyo:-

·         Sababu za watu kuzimia moyo!

·         Asizimie moyo mtu!

·         Kwanini asizimiye moyo mtu!

Sababu za watu kuzimia moyo!

Ni ukweli uliokuwa wazi kuwa Israel kama ilivyo kwa watu wengine walikuwa wamevunjika moyo na kuzimia kabisa kwa woga, mazingira waliokuwa wanakabiliana nayo, yalikuwa ni magumu na yenye kuogopesha sana, propaganda za kivita zilikuwa zimewatia hofu na kuwachosha, Goliath alikuwa akijitokeza kila siku asubuhi na jioni kwa siku 40 akiwatukana na kuwatisha sana, jambo lilolopelekea jeshi zima na mashujaa wakubwa wakiwepo kaka zake Daudi na mfalme Sauli kutishika na kufadhaika sana, Goliathi aliyatukana majeshi ya Israel waziwazi, hadharani kila mtu akishuhudia!

1Samuel 17:10-16 “Yule Mfilisti akasema, Nayatukana leo majeshi ya Israeli; nipeni mtu tupigane. Basi Sauli na Israeli wote waliposikia maneno hayo ya Mfilisti, wakafadhaika na kuogopa sana. Basi Daudi alikuwa mwana wa yule Mwefrathi, wa Bethlehemu ya Yuda, aliyeitwa jina lake Yese; naye huyo alikuwa na wana wanane; na yeye mwenyewe alikuwa mzee siku za Sauli, na mkongwe miongoni mwa watu. Nao wale wana watatu wa Yese waliokuwa wakubwa walikuwa wamefuatana na Sauli kwenda vitani, na majina ya hao wanawe watatu waliokwenda vitani ni haya, mzaliwa wa kwanza Eliabu, na wa pili wake Abinadabu, na wa tatu Shama. Naye huyo Daudi alikuwa mdogo wa wote; na hao watatu waliokuwa wakubwa wakafuatana na Sauli. Basi Daudi alikuwa akienda kwa Sauli na kurudi ili awalishe kondoo za baba yake huko Bethlehemu. Naye yule Mfilisti hukaribia asubuhi na jioni, akajitokeza siku arobaini.”

Sisi nasi katika maisha yetu tunaweza kufadhaika na kutishika na hata kuvunjika moyo kutokana na uhalisia wa changamoto, ni ukweli uliokuwa wazi kuwa Golitahi lilikuwa jitu kubwa lenye nguvu na uzoefu wa kivita, na jeshi lote la Israel lilimuogopa, yako mambo ambayo yakikupata wewe mwenyewe na hata wataalamu wanaweza kukubaliana kuwa ni jambo zito na kubwa, ikiwa una ukimwi, ikiwa una sukari, ikiwa umepatwa na kiharusi, ikiwa una kansa ya damu, ikiwa una changamoto ya ini, kansa, figo, changamoto za mfumo wa fahamu, umeme katika mwili, moyo na kadhalika ni magonjwa ya kutisha ambayo hata wataalamu wa afya wenyewe wanayaogopa na una historia yake namna na jinsi yalivyoua watu mbalimbali kwenye jamii yako, familia yako na hata majirani, changamoto za mikopo umiza, madeni ya aibu, kufilisika, hasara za namna mbalimbali, kutapeliwa fedha nyingi, kuporomoka kwa biashara, hali mbaya ya kiuchumi, kutokujitosheleza kwa mahitaji mbalimbali na umasikini wa kutisha vinaweza kuwa sababu ya kuzimia moyo, Sio hivyo tu maneno unayoyasikia kutoka upande wa upinzani au wa adui yako na wakati mwingine wanaweza hata kusema kuhusu Mungu wako kwamba tuone kama Mungu wake anaweza kumsaidia hivyo vyote vinaweza kukufanya ukazimia moyo, wakati unapokuwa katika changamoto kali na ngumu sana maneno ya adui zako yanaweza kukuumiza sana, na hata maneno ya wale watu usiowatarajia, kama wapendwa wenzetu, Yesu alipokuwa msalabani adui zale walisema pia kuhusu Mungu kwamba amemtegemea Mungu na amwokoe sasa Msalabani nasi tutamwamini maneno ya kuumiza!

Mathayo 27:40-43. “Ewe mwenye kulivunja hekalu na kulijenga kwa siku tatu, jiokoe nafsi yako; ukiwa ndiwe Mwana wa Mungu, shuka msalabani.Kadhalika na wale wakuu wa makuhani wakamdhihaki pamoja na waandishi na wazee, wakisema, Aliokoa wengine, hawezi kujiokoa mwenyewe. Yeye ni mfalme wa Israeli; na ashuke sasa msalabani, nasi tutamwamini. Amemtegemea Mungu; na amwokoe sasa, kama anamtaka; kwa maana alisema, Mimi ni Mwana wa Mungu.”

Hatupaswi kamwe kukosa imani na kuvunjika moyo au kuzimia moyo wala kuyatazama mazingira na badala yake tunapaswa kumwangalia Mungu ambaye ni mkubwa kuliko changamoto yako, Daudi kamwe hakukubali kuwa na aibu ya kitaifa na wala hakukubali Mungu wake adhalilike na ndugu zake waaibike, akiwa amejaaa Imani, uzoefu, ujuzi kuhusu Mungu na ujasiri mkubwa ambao wengi walikuwa wameupoteza yeye alisema atapambana na hali hiyo na kwa sababu hiyo asizimie moyo mtu, usizimie moyo kwaajili ya ugonjwa wako, usizimie moyo kwaajili ya adui zako, usizimie moyo kwaajili ya umasikini wako, usizimie moyo kwaajili ya changamoto na matatizo ya kifamilia, haijalishi adui anatisha kwa kiwango gani sisi tutamjia kwa jina la Bwana Mungu wa Israel aliye hai.

Asizimie moyo mtu!

Wakati kila mtu akiwa ameingiwa na hofu fadhaa na kukata tamaa au kuzimia Moyo, Daudi alikuwa na mtazamo tofauti na wengine Yeye alikuwa amejifunza kuwa Mungu ni mkubwa kuliko changamoto ya aina yoyote ile, alikuwa amejifunza na kupata uzoefu na shuhuda namna na jinsi Mungu alivyompa ushindi dhidi ya  wanyama wakali wenye nguvu kuliko binadamu wanyama kama Dubu, Simba na kadhalika alitambua kuwa Mungu alikuwa pamoja naye hata alipokuwa akiwachunga kondoo wa baba yake na kwa sababu hiyo Golitahi kwake lilikuwa ni jambo dogo sana wala sio la kufadhaisha mtu na hivyo aliwapa tumani watu wote pamoja na mfalme Asizimie moyo mtu!

1Samuel 17:34-37 “Daudi akamwambia Sauli, Mtumishi wako alikuwa akichunga kondoo za baba yake, na alipokuwa akija simba, au dubu, akamkamata mwana-kondoo wa lile kundi, mimi hutoka nikamfuata, nikampiga, nikampokonya kinywani mwake; na akinirukia, humshika ndevu zake, nikampiga, nikamwua. Mtumishi wako alimwua simba na dubu pia; na huyu Mfilisti asiyetahiriwa atakuwa kama mmoja wao, kwa sababu amewatukana majeshi ya Mungu aliye hai. Daudi akasema, Bwana aliyeniokoa na makucha ya simba, na makucha ya dubu, ataniokoa na mkono wa Mfilisti huyu. Sauli akamwambia Daudi, Enenda, na Bwana atakuwa pamoja nawe.”

Daudi aliamini kuwa sio kwa nguvu za kibinadamu atamkabili Goliath lakini ni kwa nguvu za Mungu na kwa msaada wa Mungu, alikumbuka shuhuda za ukuu wa Mungu na matendo yake na uaminifu wake, alitambua jinsi jina la Mungu linavyopaswa kutakaswa na kutukuzwa na alijua ya kuwa kwa jina hilo hakuna kinachoweza kusimama, alifahamu ya kuwa Mungu hawezi kutukanwa wala kudhalilishwa na jeuri na kiburi cha kibinadamu na kisha akakubali, Daudi alitambua kuwa kutukanwa kwa majeshi ya Mungu aliye hai ni kutukanwa kwa Mungu kwa hiyo alitaka kuitetea heshima ya Mungu, Daudi alitambua kuwa ushindi wake ni ushindi wa kitaifa na sio wa mtu mmoja na kuwa kushindwa kwa Goliathi ni kushindwa kwa wafilisti wote, Ni ukweli uliowazi katika ulimwengu wa roho vita ya Daudi na Goliati ilikuwa inawakilisha vita ya Yesu Kristo na Shetani, yule atakayeshindwa atakuwa mtumwa wa yule atakayeshindwa na watu wake na yule atakayeshinda atatawala yeye na watu wake kila mtu aliyeokoka ni mshindi kupitia ushindi wa Yesu Kristo, wakati Goliathi akiwa na kofia ya chuma na mabamba ya chuma kila mahali Daudi yeye hakuwa na kizuizi chochote na alikuwa na silaha laini yaani manati-kombeo na mawe matano tu laini

1Samuel 17:45-47.”Ndipo Daudi akamwambia yule Mfilisti, Wewe unanijia mimi na upanga, na fumo, na mkuki, bali mimi ninakujia wewe kwa jina la Bwana wa majeshi, Mungu wa majeshi ya Israeli uliowatukana. Siku hii ya leo Bwana atakuua mkononi mwangu, nami nitakupiga, na kukuondolea kichwa chako, nami leo nitawapa ndege wa angani na wanyama wa nchi mizoga ya majeshi ya Wafilisti, ili kwamba dunia nzima wajue ya kuwa yuko Mungu katika Israeli. Nao jamii ya watu wote pia wajue ya kwamba Bwana haokoi kwa upanga wala kwa mkuki; maana vita ni vya Bwana, naye atawatia ninyi mikononi mwetu.”

Wakati Goliathi alikuwa akitema propaganda tu na vitisho kwa kujiamini kwa kiburi na majivuno, Daudi alikuwa akizitamka shuhuda za Mungu na ukweli wa neno lake Mungu na uweza wake, ni ukweli ulio wazi kuwa siku ile Daudi alimpiga Goliathi na kwa kutumia upanga wa Goliathi mwenyewe alikata kichwa chake, tukio hili liliwapa nguvu Israel na waliwakimbiza wafilisti na kuwachinja kama walivyotaka na kujikusanyia nyara:-

1Samuel 17:48-52 “Ikawa, hapo Mfilisti alipojiinua, akaenda akamkaribia Daudi, ndipo Daudi naye akapiga mbio, akalikimbilia jeshi ili akutane na yule Mfilisti. Daudi akatia mkono wake mfukoni, akatwaa humo jiwe moja, akalitupa kwa kombeo lake, akampiga Mfilisti katika kipaji cha uso; jiwe hilo likamwingilia kipajini, akaanguka chini kifudifudi. Hivyo Daudi akamshinda yule Mfilisti kwa kombeo na jiwe, akampiga Mfilisti, akamwua; walakini Daudi hakuwa na upanga mkononi mwake. Ndipo Daudi akapiga mbio, akasimama juu ya Mfilisti, akautwaa upanga wake, akaufuta alani mwake, akamwua, akamkata kichwa kwa upanga huo. Nao Wafilisti walipoona ya kuwa shujaa wao amekufa, wakakimbia. Nao watu wa Israeli na wa Yuda wakainuka, na kupiga kelele, nao wakawafuata Wafilisti mpaka ufikapo Gathi, na mpaka malango ya Ekroni. Nao majeruhi wa Wafilisti wakaanguka kando ya njia iendayo Shaarimu, mpaka Gathi, na mpaka Ekroni.”  
           

Kwanini asizimiye moyo mtu!

Daudi alikuwa na ufahamu kuwa ushindi wake hautokani na yeye mwenyewe bali ushindi wake unatokana na Mungu, sisi nasi hatuna budi kufahamu kwamba ushindi wetu unapatikana kupitia Yesu Kristo ambaye alishinda kifo na mauti, ushindi wowote tulio nao na tutakaokuwa nao ni ushindi unaotokana na ushindi wake Kristo Yesu mwana wa Daudi.  

1Wakorintho 15:57 “Lakini Mungu na ashukuriwe atupaye kushinda kwa Bwana wetu Yesu Kristo.”

Maandiko yanatukumbusha tu kuwa hakuna changamoto kubwa kuliko Mungu wetu, kila mtu aliyeokolewa na anayemtegemea Mungu anapaswa kumtegemea Mungu na kumfanya kuwa ngao yake na kinga yake, tunapaswa kuwa na ujasiri na kuacha kupoteza matumaini, hatupaswi kamwe kuzimia moyo kama tumemfanya Bwana kuwa ngao yetu, hatupaswi kulia wala kufadhaika maana Mungu ndiye wokovu wetu, na ngome yetu na hakuna wa kutukaribia wala kutudhuru vyovyote vile!

Zaburi 27:1-3 “Bwana ni nuru yangu na wokovu wangu, Nimwogope nani? Bwana ni ngome ya uzima wangu, Nimhofu nani? Watenda mabaya waliponikaribia, Wanile nyama yangu, Watesi wangu na adui zangu, Walijikwaa wakaanguka. Jeshi lijapojipanga kupigana nami, Moyo wangu hautaogopa. Vita vijaponitokea, Hata hapo nitatumaini.”

Maandiko yanatukumbusha kuwa Mungu hutumia mambo manyonge sana, wakati ambapo Goliath anaonekana kuwa na silaha bora, mkuki mkubwa na uzoefu mkubwa vitani, huku mwili wake umezingirwa na mambamba ya shaba Daudi alikuwa ni kijana mdogo, mzuri macho mekundu lakini alijikinga kwa jina la Mungu na kumfanya Mungu kuwa tumaini lake, hii inatukumbusha kuwa Mungu anaweza kutumia chochote na kumtumia mtu yeyote bila kujali hali yake, historia yake na muonekano wake wa nje, unyonge wake au kupuuzwa kwake, Mungu hutumia vilivyodharaulika!  

1Wakorintho 1:26-29 “Maana, ndugu zangu, angalieni mwito wenu, ya kwamba si wengi wenye hekima ya mwilini, si wengi wenye nguvu, si wengi wenye cheo walioitwa; bali Mungu aliyachagua mambo mapumbavu ya dunia awaaibishe wenye hekima; tena Mungu alivichagua vitu dhaifu vya dunia ili aviaibishe vyenye nguvu; tena Mungu alivichagua vitu vinyonge vya dunia na vilivyodharauliwa, naam, vitu ambavyo haviko, ili avibatilishe vile vilivyoko; mwenye mwili awaye yote asije akajisifu mbele za Mungu.”

Maandiko yanatukumbusha kuwa Mungu ni mwaminifu na kuwa tunapokabiliana na changamoto za aina yoyote katika maisha yetu na tukumbuke namna na jinsi alivyotusaidia katika mambo mengine kumbuka matendo yake ya kale na hii itamuimarisha kila mmoja wetu kujua kuwa Mungu yule yule asiyebadilika aliyewasaidia baba zetu katika vita zao atajitokeza tena kwa namna nyingine kutusaidia

Zaburi 77:11-14 “Nitayakumbuka matendo ya Bwana; Naam, nitayakumbuka maajabu yako ya kale. Pia nitaitafakari kazi yako yote; Nitaziwaza habari za matendo yako. Ee Mungu, njia yako i katika utakatifu; Ni nani aliye mungu mkuu kama Mungu? Wewe ndiwe Mungu ufanyaye maajabu; Uliudhihirisha uweza wako kati ya mataifa.”

Ee Bwana usimuache msomaji wangu, na msikilizaji wangu na kila mtu duniani anayekutegemea wewe, usimwache akazimia moyo wakati wa taabu yake lakini umpe moyo wa ujasiri kama Daudi na nutupe ushindi katika vita zetu za maisha katika jina la Yesu Kristo amen!

Na. Rev Innocent Samuel Kamote.

Mkuu wa wajenzi mwenye Hekima!

Jumapili, 6 Julai 2025

Yesu Kristo kwa mabadiliko ya jamii!

 


1Timotheo 1:15-16 “Na neema ya Bwana wetu ilizidi sana, pamoja na imani na pendo lililo katika Kristo Yesu. Ni neno la kuaminiwa, tena lastahili kukubalika kabisa, ya kwamba Kristo Yesu alikuja ulimwenguni awaokoe wenye dhambi; ambao wa kwanza wao ni mimi. Lakini kwa ajili hii nalipata rehema, ili katika mimi wa kwanza, Yesu Kristo audhihirishe uvumilivu wake wote; niwe kielelezo kwa wale watakaomwamini baadaye, wapate uzima wa milele.”




Utangulizi:

Ni muhimu kujikumbusha kuwa Yesu Kristo mwana wa Mungu alikuja duniani kwa kusudi la kutafuta na kuokoa kile kilichopotea, Maisha yake na huduma yake pamoja na mafundisho yake yalileta mabadiliko makubwa sana ya kiroho na kijamii na uadilifu katika maisha ya watu wengi, mtu mmoja mmoja na jamii kwa ujumla.

Luka 19:2-10 “Na tazama, palikuwa na mtu, jina lake Zakayo, mkubwa mmoja katika watoza ushuru, naye ni tajiri. Huyu alikuwa akitafuta kumwona Yesu ni mtu wa namna gani, asiweze kwa sababu ya umati wa watu, maana ni mfupi wa kimo. Akatangulia mbio, akapanda juu ya mkuyu apate kumwona, kwa kuwa atakuja kuipitia njia ile. Na Yesu, alipofika mahali pale, alitazama juu, akamwambia, Zakayo, shuka upesi, kwa kuwa leo imenipasa kushinda nyumbani mwako. Akafanya haraka, akashuka, akamkaribisha kwa furaha. Hata watu walipoona, walinung'unika wote, wakisema, Ameingia kukaa kwa mtu mwenye dhambi.Zakayo akasimama, akamwambia Bwana, Tazama, Bwana, nusu ya mali yangu nawapa maskini, na ikiwa nimenyang'anya mtu kitu kwa hila namrudishia mara nne. Yesu akamwambia, Leo wokovu umefika nyumbani humu, kwa sababu huyu naye ni mwana wa Ibrahimu. Kwa kuwa Mwana wa Adamu alikuja kutafuta na kuokoa kile kilichopotea.”

Alipokuwa duniani Yesu alijichanganya na kuwaendea wenye dhambi kwa upendo heshima na kwa unyenyekevu mkubwa sana na kuwafanya wao wampende na kumkubali, aliyabadilisha maisha yao wakati mwingine wala sio kwa kuhubiri kwa nguvu bali kwa kuwaonyesha upendo na kuwajali hususani wale waliokuwa wamekataliwa na kuonekana kuwa hawafai, wapinzani wake wa kidini walimshutumu sana wakifiri ya kuwa alikuwa ni  nabii aliyekosa kiasi kwa kuwa alikaa na kula na kuongea na wenye dhambi, majibu yake kwa wapinzani wake yalikuwa yamejaa hekima neema na mshangazo mkubwa sana kwani pia yalionyesha kuwa alikuwa na ujuzi na mpango mkakati aliokuja nao ambao ni kuleta tiba kwa wenye dhambi ambao walikuwa wakitubu kwa njia nyepesi sana na kupokea muujiza mkubwa muujiza wa mabadiliko ya kitabia akijibainisha hivyo Yesu alisema

Luka 5:29-32 “Na Lawi akamfanyia karamu kubwa nyumbani mwake; palikuwa na mkutano mkuu wa watoza ushuru na watu wengineo waliokuwa wameketi chakulani pamoja nao. Ikawa Mafarisayo na waandishi wao kuwanung'unikia wanafunzi wake, wakisema, Mbona mnakula na kunywa pamoja na watoza ushuru na wenye dhambi? Yesu akajibu akawaambia, Wenye afya hawana haja na tabibu, isipokuwa walio hawawezi. Sikuja kuwaita wenye haki, bali wenye dhambi, wapate kutubu.”

Majibu yake Yesu na maneno yake na matendo yanadhihirisha wazi kuwa Yesu Kristo alikuja duniani akiwa na mpango na mkakati wa kuleta mabadiliko makubwa kwa jamii, Yesu anasifiwa kama mojawapo ya wanafalsafa wakubwa sana duniani lakini moja ya sifa yake kubwa inayomtofautisha na wanafalsafa wengine ni uwezo wake wa kubadilisha maisha ya watu, kwa muda wa miaka zaidi ya 2000 kumekuwepo na wanafunzi wengi sana wa Bwana Yesu na wanaoonyesha msimamo na mabadiliko makubwa ya kimaisha ya wale waliokutwa na mafundisho yake hii maana yake ni kwamba hata pamoja na kuwa amepaa mbinguni habari zake njema zimekuwa njema na dawa ya kipekee kwa jamii kwa hiyo ni wazi kuwa mtu yeyote ayayehitaji mabadiliko ya mtindo wa maisha na ikawa imeshindikana sehemu nyingine anamuhitaji Yesu,  na sisi nasi kama watumishi wake hatuna budi kumuuza Yesu kwa kumtangaza na kumuhubiri katika jamii kwaajili ya mabadiliko ya kweli ya jamii yetu “Yesu Kristo kwa mabadiliko ya jamii!”, tutajifunza somo hili Yesu kwa mabadiliko ya jamii kwa kuzingatia vipengele vitatu vifuatavyo:-

·         Yesu alikuja kutafuta na kuokoa kile kilichopotea.

·         Mifano ya watu waliokutana na Yesu na kubadilika.

·         Yesu Kristo kwa mabadiliko ya jamii!.


Yesu alikuja kutafuta na kuokoa kile kilichopotea

Kama tulivyoona katika utangulizi wa somo hili ya kuwa Yesu Kristo alikuja duniani akiwa na mpango mkakati ulio wazi ambao ni kuokoa kile kilichopotea, Kimsingi Yesu alikuja kusamehe watu dhambi na kuyabadili maisha yao kabisa, alitajwa mapema katika maandiko kwamba yeye ndiye atakayewaokoa watu wake na dhambi zao na pamoja na matokeo hasi yaliyosababishwa na dhambi

Mathayo 1:21-23 “Naye atazaa mwana, nawe utamwita jina lake Yesu, maana, yeye ndiye atakayewaokoa watu wake na dhambi zao. Hayo yote yamekuwa, ili litimie neno lililonenwa na Bwana kwa ujumbe wa nabii akisema, Tazama, bikira atachukua mimba, Naye atazaa mwana; Nao watamwita jina lake Imanueli; Yaani, Mungu pamoja nasi.”

Luka 19:9-10 “Yesu akamwambia, Leo wokovu umefika nyumbani humu, kwa sababu huyu naye ni mwana wa Ibrahimu.Kwa kuwa Mwana wa Adamu alikuja kutafuta na kuokoa kile kilichopotea.”

Watu wote duniani wanafahamu kuwa ni makosa kumteda Mungu dhambi na ndani ya mioyo yao wanajua na wako ambao wanajitahidi kwa jitihada zao za kidini na kiimani lakini wanashindwa, dhambi ni adui mkubwa wa mwanadamu analeta hatia na kuondoa ujasiri katika moyo, Dhambi pia inaweza ikakufanya uishi kinafiki bila kupenda, inatawala na kuwafanya watu kuwa watumwa. Dhambi ni adui yetu mkubwa kama alivyo shetani tu, tangu anguko la mwanadamu duniani asili ya mwanadamu imeathiriwa na dhambi na kwa sababu hiyo wanadamu hawawezi kufanya yale wanayoyapenda ikiwa ni pamoja na kumpendeza Mungu, umasikini wa kiroho  na ukosefu wa tumaini umeingia, uhusiano na Mungu umeingia mashakani na mwanadamu anapotea akijiona, Ni Yesu Kristo peke yake aliyekuja kurejesha tumaini hilo, Ni yeye pekee aliyekuja kuonyesha upendo wa Mungu kwetu  na kwa njia ya msalaba aliikamilisha kazi hiyo pana kwa sababu hiyo sasa mlango uko wazi kwa jamii nzima, waliokataliwa, walevi, wachawi, makahaba, wagonjwa, na jamii nzima inayotumikishwa bila kupenda tunapaswa kuitumia huruma ya Mungu wetu kwa kuukubali upendo wake na kazi yake aliyoifanya pale msalabani ili tusipotee, wajibu wetu mkubwa ni kumwamini na tukimwamini hatutapotea na badala yake tutakuwa na uzima wa milele.

Yohana 3:16-18 “Kwa maana jinsi hii Mungu aliupenda ulimwengu, hata akamtoa Mwanawe pekee, ili kila mtu amwaminiye asipotee, bali awe na uzima wa milele. Maana Mungu hakumtuma Mwana ulimwenguni ili auhukumu ulimwengu, bali ulimwengu uokolewe katika yeye. Amwaminiye yeye hahukumiwi; asiyeamini amekwisha kuhukumiwa; kwa sababu hakuliamini jina la Mwana pekee wa Mungu.”

Mifano ya watu waliokutana na Yesu na kubadilika.

Alipokuwa duniani mwokozi Yesu Kristo alisababisha mabadiliko makubwa sana ambayo yanaendelea mpaka leo kila inapohubiriwa injili na watu wakaikubali, Yesu alikuwa Mwalimu wa kipekee ambaye hakufundisha tu bali mafundisho yake yalikuwa na nguvu na mamlaka yakiambatana na uwezo mkubwa wa kubadilisha maisha ya watu hata wale waliokuwa wagumu kufikika, Yesu alibadilisha kila mtu aliyekutana naye na akawapa maisha mapya na hapa iko mifano kadhaa:-

1.       Paulo mtume - alikuwa moja ya watu hatari sana mtu mwenye msimamo mkali katika dini yake aliyekuwa anaiona imani ya kikrito kama imani potofu na inayoharibu mila na tamaduni za kiyahudi kwa hiyo alitumia nguvu zake zote kuipinga na kuipiga vita imani hii, alisimamia mauaji ya Stephano, na kwa hiyari yake aliomba kibali kwa kuhani mkuu kuwafuatia na kuwakamata watu wote wa njia hii yaani (Waliookoka) na kuwaburuza na kuwatia ndani.

 

Matendo 7:16-18 “Wakapiga kelele kwa sauti kuu, wakaziba masikio yao, wakamrukia kwa nia moja, wakamtoa nje ya mji, wakampiga kwa mawe. Nao mashahidi wakaweka nguo zao miguuni pa kijana mmoja aliyeitwa Sauli.Wakampiga kwa mawe Stefano, naye akiomba, akisema, Bwana Yesu, pokea roho yangu.Akapiga magoti, akalia kwa sauti kuu, Bwana, usiwahesabie dhambi hii. Akiisha kusema haya akalala. Na Sauli alikuwa akiona vema kwa kuuawa kwake.”

 

Matendo 9:1-5 “Lakini Sauli, akizidi kutisha na kuwaza kuwaua wanafunzi wa Bwana, akamwendea Kuhani Mkuu, akataka ampe barua za kuenda Dameski zilizoandikwa kwa masinagogi, ili akiona watu wa Njia hii, waume kwa wake, awafunge na kuwaleta Yerusalemu. Hata alipokuwa akisafiri, ikawa anakaribia Dameski; ghafula ikamwangaza kote kote nuru kutoka mbinguni. Akaanguka chini, akasikia sauti ikimwambia, Sauli, Sauli, mbona waniudhi? Akasema, U nani wewe, Bwana? Naye akasema, Mimi ndimi Yesu unayeniudhi wewe.”

 

Mtume Paulo aliyekuwa wa ajabu na adui mkubwa sana wa ukristo alipokutana na Yesu mabadiliko makubwa sana yalitokea maishani mwake na uadui wake dhidi ya Yesu Kristo na kanisa lake ulifikia mwisho na badala ya kuhukumiwa kuuawa Yesu alimuamuru kuwa chombo chake cha kuihubiri injili na akawa mtu mwenye bidii na juhudi kubwa na kuleta mchango mkubwa sana katika jamii, yeye anakumbuka jinsi Mungu alivyomuokoa na baadaye maisha yake yakawa kielelezo kwa jamii ya wakati ule na sasa.

 

1Timotheo 1:154-16 “Na neema ya Bwana wetu ilizidi sana, pamoja na imani na pendo lililo katika Kristo Yesu. Ni neno la kuaminiwa, tena lastahili kukubalika kabisa, ya kwamba Kristo Yesu alikuja ulimwenguni awaokoe wenye dhambi; ambao wa kwanza wao ni mimi. Lakini kwa ajili hii nalipata rehema, ili katika mimi wa kwanza, Yesu Kristo audhihirishe uvumilivu wake wote; niwe kielelezo kwa wale watakaomwamini baadaye, wapate uzima wa milele.”

 

2.       Mwanamke msamaria – Alikuwa ni mwanamke ambaye ametengwa na jamii kwa sababu ya maisha yake ya aibu, hata muda wake wa kutembea na kwenda kuteka maji ulikuwa ni muda wa tofauti na wanawake wenzake kijijini, Yesu alipokutana naye alizungumza naye moja kwa moja na akaweza kushughulika na hali yake ya kiroho kimwili na kisaikolojia alimponya na kuitimiza kiu yake ya kuhitaji maji ya uzima, baada ya muda mfupi wa kukutana na Yesu na kuzungumza naye na kumfunulia yaliyokuwa yakiendelea moyoni mwake mwanamke huyu aligeuka muhubiri wa injili ambaye aliwavuta wengi kuja kwa Yesu maisha yake  yalibadilika na kupitia yeye jamii yake pia ilipata mwanga wa injili na giza likaondoka katika mji wao.

 

Yohana 4:3-42 “aliacha Uyahudi, akaenda zake tena mpaka Galilaya. Naye alikuwa hana budi kupita katikati ya Samaria. Basi akafika kunako mji wa Samaria, uitwao Sikari, karibu na lile shamba ambalo Yakobo alimpa Yusufu mwanawe. Na hapo palikuwa na kisima cha Yakobo. Basi Yesu, kwa sababu amechoka kwa safari yake, akaketi vivi hivi kisimani. Nayo ilikuwa yapata saa sita. Akaja mwanamke Msamaria kuteka maji. Yesu akamwambia, Nipe maji ninywe. Kwa maana wanafunzi wake wamekwenda mjini kununua chakula. Basi yule mwanamke Msamaria akamwambia, Imekuwaje wewe Myahudi kutaka maji kwangu, nami ni mwanamke Msamaria? (Maana Wayahudi hawachangamani na Wasamaria.) Yesu akajibu, akamwambia, Kama ungaliijua karama ya Mungu, naye ni nani akuambiaye, Nipe maji ninywe, ungalimwomba yeye, naye angalikupa maji yaliyo hai. Yule mwanamke akamwambia, Bwana, huna kitu cha kutekea, na kisima ni kirefu; basi umeyapata wapi hayo maji yaliyo hai? Je! Wewe u mkubwa kuliko baba yetu, Yakobo, aliyetupa kisima hiki, naye mwenyewe akanywa maji yake, na wanawe pia, na wanyama wake? Yesu akajibu, akamwambia, Kila anywaye maji haya ataona kiu tena;  walakini ye yote atakayekunywa maji yale nitakayompa mimi hataona kiu milele; bali yale maji nitakayompa yatakuwa ndani yake chemchemi ya maji, yakibubujikia uzima wa milele. Yule mwanamke akamwambia, Bwana, unipe maji hayo, nisione kiu, wala nisije hapa kuteka. Yesu akamwambia, Nenda kamwite mumeo, uje naye hapa. Yule mwanamke akajibu, akasema, Sina mume. Yesu akamwambia, Umesema vema, Sina mume; kwa maana umekuwa na waume watano, naye uliye naye sasa siye mume wako; hapo umesema kweli. Yule mwanamke akamwambia, Bwana, naona ya kuwa u nabii! Baba zetu waliabudu katika mlima huu, nanyi husema ya kwamba huko Yerusalemu ni mahali patupasapo kuabudia. Yesu akamwambia, Mama, unisadiki, saa inakuja ambayo hamtamwabudu Baba katika mlima huu, wala kule Yerusalemu. Ninyi mnaabudu msichokijua; sisi tunaabudu tukijuacho; kwa kuwa wokovu watoka kwa Wayahudi.Lakini saa inakuja, nayo sasa ipo, ambayo waabuduo halisi watamwabudu Baba katika roho na kweli. Kwa maana Baba awatafuta watu kama hao wamwabudu. Mungu ni Roho, nao wamwabuduo yeye imewapasa kumwabudu katika roho na kweli. Yule mwanamke akamwambia, Najua ya kuwa yuaja Masihi, (aitwaye Kristo); naye atakapokuja, yeye atatufunulia mambo yote. Yesu akamwambia, Mimi ninayesema nawe, ndiye. Mara hiyo wakaja wanafunzi wake, wakastaajabu kwa sababu alikuwa akisema na mwanamke; lakini hakuna aliyesema, Unatafuta nini? Au, Mbona unasema naye? Basi yule mwanamke akauacha mtungi wake, akaenda zake mjini, akawaambia watu, Njoni, mtazame mtu aliyeniambia mambo yote niliyoyatenda. Je! Haimkini huyu kuwa ndiye Kristo? Basi wakatoka mjini, wakamwendea. Huko nyuma wanafunzi wakamsihi wakisema, Rabi, ule. Akawaambia, Mimi ninacho chakula msichokijua ninyi. Basi wanafunzi wake wakasemezana, Je! Mtu amemletea chakula?  Yesu akawaambia, Chakula changu ndicho hiki, niyatende mapenzi yake aliyenipeleka, nikaimalize kazi yake. Hamsemi ninyi, Bado miezi minne, ndipo yaja mavuno? Tazama, mimi nawaambieni, Inueni macho yenu myatazame mashamba, ya kuwa yamekwisha kuwa meupe, tayari kwa mavuno. Naye avunaye hupokea mshahara, na kukusanya matunda kwa uzima wa milele, ili yeye apandaye na yeye avunaye wapate kufurahi pamoja. Kwa maana hapo neno hilo huwa kweli, Mmoja hupanda akavuna mwingine. Mimi naliwatuma myavune yale msiyoyataabikia; wengine walitaabika, nanyi mmeingia katika taabu yao. Na katika mji ule Wasamaria wengi walimwamini kwa sababu ya neno la yule mwanamke, aliyeshuhudia kwamba, Aliniambia mambo yote niliyoyatenda. Basi wale Wasamaria walipomwendea, walimsihi akae kwao; naye akakaa huko siku mbili. Watu wengi zaidi wakaamini kwa sababu ya neno lake. Wakamwambia yule mwanamke, Sasa tunaamini, wala si kwa sababu ya maneno yako tu; maana sisi tumesikia wenyewe, tena twajua ya kuwa hakika huyu ndiye Mwokozi wa ulimwengu.”

 

Ushuhuda wa mwanamke msamaria unatukumbusha kazi ya Yesu ya kubadilisha jamii, na tunajifunza jinsi ambavyo hata mtu mmoja tu aliyedharauliwa na kukataliwa katika jamii na ambaye anaonekana hafai anaweza kabisa kubadilika na kusababisha mabadiliko makubwa kwa jamii, Yesu anabadilisha maisha, Yesu anabadilisha tabia, Yesu anabadilisha jamii.

 

3.       Mathayo yule mtoza ushuru – Watoza ushuru walikuwa  mojawapo ya kundi lililochukiwa na watu katika jamii ya wayahudi, kwanza wakihesabika kama wasaliti kwa sababu walitoza kodi watu wa taifa lao kwa niaba ya taifa la kigeni au la kikoloni la Warumi, lakini pia walionekana kama kundi la watu wenye kudhulumu au wezi kwa sababu walijikusanyia mali kwa dhuluma au kujitajirisha kwa fedha za haramu, kwa hiyo mafarisayo waliwaweka katika kundi moja la watu najisi na wasiofaa  na kudharaulika au kuonekana kama ni wadhambi ona

 

Luka 18:9-14 “Akawaambia mfano huu watu waliojikinai ya kuwa wao ni wenye haki, wakiwadharau wengine wote. Watu wawili walipanda kwenda hekaluni kusali, mmoja Farisayo, wa pili mtoza ushuru. Yule Farisayo akasimama akiomba hivi moyoni mwake; Ee Mungu, nakushukuru kwa kuwa mimi si kama watu wengine, wanyang'anyi, wadhalimu, wazinzi, wala kama huyu mtoza ushuru. Mimi nafunga mara mbili kwa juma; hutoa zaka katika mapato yangu yote. Lakini yule mtoza ushuru alisimama mbali, wala hakuthubutu hata kuinua macho yake mbinguni, bali alijipiga-piga kifua akisema, Ee Mungu, uniwie radhi mimi mwenye dhambi. Nawaambia, huyu alishuka kwenda nyumbani kwake amehesabiwa haki kuliko yule; kwa maana kila ajikwezaye atadhiliwa, naye ajidhiliye atakwezwa.”

 

Tofauti na mafarisayo ambao waliwabagua sana watoza ushuru na kujihesabia haki Yesu yeye aliwaendea na kuwafanya rafiki zake akila na kufurahi pamoja nao ili hatimaye awabadilishe maisha yao akiwepo Mathayo ambaye baadaye Yesu alimtumia kuandika injili

 

Mathayo 9:9-13 “Naye Yesu alipokuwa akipita kutoka huko aliona mtu ameketi forodhani, aitwaye Mathayo, akamwambia, Nifuate. Akaondoka, akamfuata. Ikawa alipoketi nyumbani ale chakula, tazama, watoza ushuru wengi na wenye dhambi walikuja wakaketi pamoja na Yesu na wanafunzi wake. Mafarisayo walipoona, waliwaambia wanafunzi wake, Mbona mwalimu wenu anakula pamoja na watoza ushuru na wenye dhambi? Naye aliposikia, aliwaambia, Wenye afya hawahitaji tabibu, bali walio hawawezi. Lakini nendeni, mkajifunze maana yake maneno haya, Nataka rehema, wala si sadaka; kwa maana sikuja kuwaita wenye haki, bali wenye dhambi.”

Mifano hii inatuthibitishia na kutuonyesha ya kwamba ni Yesu peke yake anayeweza kuleta mabadiliko ya kweli katika jamii, na ni mabadiliko yanayoanzia moyoni na yasiyo na unafiki yanayotokana na njia yake ya kuuendea ulimwengu kwa upendo na huruma na nguvu za Mungu, kwa hiyo kupitia upendo wake huu aliweza kuwafikishia watu maisha mapya bila kutumia nguvu aliwagusa watu kwa neema yake na upendo wake  na kuwapa maisha mapya yaliyoathiri jamii zao, hakuna mtume wala nabii yeyote ambaye alikuwa au amakuwa na uwezo wa kuyabadili maisha ya watu wake na kuwafanya kuwa wema kama ilivyo kwa Bwana wetu Yesu Kristo!.

Kwa msingi huo tunajifunza ya kwamba hata sasa tunaweza kumpeleka Yesu kwa jamii na kumnadi kama biashara inayoweza kuleta mabadiliko ya kila aina katika maisha yetu, Yesu atabadilisha maisha ya watu kutoka kwenye uhalifu kuwa watu wema, kutoka kuwa wavuvi wa samaki kuwa wavuvi wa watu, kutoka kwenye kundi la kudharaulika kwenda kwenye kundi la kuheshimika na kutoka kwenye huzuni kwenda kwenye furaha, kanisa nini tunapaswa kukifanya ni kuuza bidhaa Yesu na kuitangaza kwa ajili ya mabadiliko ya jamii!, Kama alivyobadilisha wengine anaweza kumbadilisha yeyote  yule hata ambaye anaonekana kushindikana katika jamii, kama unaona ya kuwa jamii ni kama imekuchoka kwa maneno na matendo yako Jaribu Yesu Kristo leo na utafurahi

Yesu Kristo kwa mabadiliko ya jamii!

Katika jamii hii tuliyo nayo ambayo inakabiliwa na changamoto nyingi ikiwa ni pamoja na ufisadi, ukosefu wa haki, dhuluma uhalifu, umasikini, unyonge, mmomonyoko wa maadili, kukata tamaa na msongo wa mawazo dunia inahitaji sana ujumbe wa Yesu Kristo ambao ndio pekee unaobaki kuwa tiba ya kweli ya changamoto hizi ni lazima tuwapelekee watu bidhaa hii na kuinadi kwao, Yesu Kristo kwa mabadiliko ya jamii, ni yeye pekee ambaye anatoa mwaliko wa kuwapoza watu wote wenye kuelemewa na mizigo na kutoa ahadi ya kweli kwamba atawapumzisha!

Mathayo 11:28-30 “Njoni kwangu, ninyi nyote msumbukao na wenye kulemewa na mizigo, nami nitawapumzisha. Jitieni nira yangu, mjifunze kwangu; kwa kuwa mimi ni mpole na mnyenyekevu wa moyo; nanyi mtapata raha nafsini mwenu; kwa maana nira yangu ni laini, na mzigo wangu ni mwepesi.”

Yesu anauwezo wa kubadilisha mioyo ya wanadamu wote katika jamii mabadiliko ya watu kama mwanamke msamaria, mabadiliko ya watu walioshikilia dini zao kama Paulo na mabadiliko ya watu waliokataliwa na jamii kama kina Mathayo na Zakayo na mwanamke Msamaria,  tukiwakutanisha na watu wa jinsi hiyo na Yesu watapewa pumziko la kweli na maisha ya haki upendo na huruma zake

Kila mwanadamu aliyepoteza tumaini na kukata tamaa katika jamii na anayehitaji kushinda changamoto za kila siku za maisha ni aelewe na ajuzwe kuwa ni Yesu Kristo pekee anayeweza kurejesha matumaini hayo, yeye pekee huelekeza watu kuishi maisha ya haki na kutoa mwongozo wa maisha yanayoweza kubadilisha jamii, hutumii nguvu zako kubadilika Ni Yesu anatumia damu yake na neema yake na trehema zake kukubadilisha wewe unacho kihitaji ni Yesu tu!

Kwa hiyo ni lazima tumuhubiri Yesu na kumpeleka Yesu kwa jamii yenye changamoto za aina mbalimbali tunaelezwa kuwa nyakati za kanisa la kwanza wahubiri hawakuwa na ujumbe mwingine zaidi walimuhubiri Yesu Kristo hawakuhubiri watu wala madhehebu yao wala makanisa yao lakini walimuhubiri Yesu Kristo; Muhubiri Yesu tangaza bidhaa hii ieleze jamii Yesu Kristo kwa mabadiliko, tukitaka kuwapelekea watu furaha ya kweli wapelekee Yesu, wahubiri watu kuhusu Yesu waelekeze watu kwa Yesu, wape watu bidhaa iitwayo Yesu Kristo; Yesu ndio sera inayouzika kuliko sera nyingine hakuna mbadala  wa Yesu, Damu yake inatakasa, yeye mwenyewe yuko hai ameketi mkono wa kuume wa Mungu waelezee watu kuhusu Yesu; Yesu anaokoa, Yesu anaponya, Yesu anabadilisha maisha analeta tumaini, Yesu anatakasa, Yesu anasamehe, Yesu habadiliki, Yesu haukumu mtu,Yesu ni mwaminifu, Yesu amejaa neema na rehema na huruma hakua kama Yesu; Yesu ni yeye yule jana leo na hata milele, tumuuze Yesu, tumnadi yetu, Tangaza uza bidhaa Yesu kwa mabadiliko ya jamii

Matendo 8:5-8 “Filipo akatelemka akaingia mji wa Samaria, AKAWAHUBIRI KRISTO. Na makutano kwa nia moja wakasikiliza maneno yale yaliyosemwa na Filipo walipoyasikia na kuziona ishara alizokuwa akizifanya. Kwa maana pepo wachafu wakawatoka wengi waliopagawa nao, wakilia kwa sauti kuu; na watu wengi waliopooza, na viwete, wakaponywa. Ikawa furaha kubwa katika mji ule.” 

Yesu Kristo alikuja kutafuta na kuokoa kile kilichopotea, na ni kupitia maisha yake na huduma yake na kazi yake aliyoifanya pale msalabani alibadilisha maisha ya watu na anabadilisha maisha ya watu hata leo ikiwa jamii yoyote inahitaji Amani na furaha basi jamii hiyo inapaswa kumpokea Yesu, upendo wake, kujali kwake huruma yake na nguvu zake ziko kutusaidia jamii yetu kwa sasa inamuhitaji  Yesu zaidi kuliko kitu kingine chochote atawaokoa na kuwasamehe na kuwapoza mioyo yao na kuwaletea nyakati za kuburudishwa, na kuwapoza mioyo yao na kuishusha mizigo yao!

Zaburi 107:13-15 “Wakamlilia Bwana katika dhiki zao, Akawaponya na shida zao. Aliwatoa katika giza na uvuli wa mauti, Akayavunja mafungo yao. Na wamshukuru Bwana kwa fadhili zake, Na maajabu yake kwa wanadamu.”

2Wakorintho 5:17 “Hata imekuwa, mtu akiwa ndani ya Kristo amekuwa kiumbe kipya; ya kale yamepita tazama! Yamekuwa mapya.”

Haijalishi maisha yako yameharibiwa kwa kiasi gani, haijalishi ulirogwa kwa mchawi gani, haijalishi adui zako wametambikia kwa kiwango gani,  kutano moja tu na Bwana Yesu litabadilisha maisha yako na mabadiliko makubwa yatakuwa ushahidi kwako, unamuhitaji Yesu kwa mabadiliko ya maisha yako leo,  mpe Yesu maisha yako na hutakuwa mtu yule tena, maisha yoyote bila Yesu ni maisha yasiyokamilika,  maisha yoyote bila Yesu ni maisha yenye kusikitisha sana, Maisha yoyote bila Yesu ni maisha yenye upungufu, Kila mmoja wetu anamuhitaji Yesu, tunamuhitaji hata kwa ushindi wa vita zetu, tunamuhitaji pia kwaajili ya maisha yetu yajayo, tunamuhitaji katika ndoa zetu, kazini kwetu, biashara zetu, masomo yetu  na popote, yeye hubadilisha maisha! Jaribu leo!, omba sala hii pamoja nami endapo liko eneo katika maisha yako unahitaji mabadiliko! Tuombe!

Bwana kama iekupendeza wewe kutubadilisha sisi, Basi nakuomba tufanye kuwa mtu yule ambaye ungependa tuwe, tunatamani kubadilika, kwa sababu hiyo mpe neema kila mmoja kuwa vile upendavyo wewe, nakushukuru kwa sababu utawabadilisha wengi, hata Msomaji wangu na msikilizaji wangu utampa kuona wema wako, asante kwa sababu utafanya zaidi ya jinsi nilivyokuomba kwa unyenyekevu mkubwa katika jina la Yesu Kristo Amen!

Na Rev. Innocent Samuel Kamote

Mkuu wa wajenzi mwenye Hekima

Jumapili, 29 Juni 2025

Rahabu yule kahaba!


Yoshua 6:22-25. “Naye Yoshua akawaambia wale wanaume wawili walioipeleleza nchi, Ingieni katika nyumba ya yule kahaba, mkamtoe huyo mwanamke mwenyewe na vitu vyote alivyo navyo, kama mlivyomwapia. Basi wale vijana wapelelezi wakaingia, wakamtoa Rahabu, na baba yake, na mama yake, na ndugu zake, na vitu vyote walivyokuwa navyo, wakawatoa na jamaa zake wote pia; wakawaweka nje ya matuo ya Israeli. Kisha wakauteketeza mji kwa moto, na vitu vyote vilivyokuwa ndani yake; bali fedha, na dhahabu, na vyombo vya shaba, na vya chuma, wakavitia katika hazina ya nyumba ya Bwana. Lakini Yoshua akamhifadhi Rahabu, yule kahaba, na watu wa nyumba ya baba yake, na vitu vyote alivyokuwa navyo; naye akakaa kati ya Israeli hata leo; kwa sababu aliwaficha wale wajumbe aliowatuma Yoshua ili kuupeleleza mji wa Yeriko.”




Utangulizi:

Hakuna mtu mbaya sana, wala hakuna mtu aliye mbali sana kiasi cha Rehema za Mungu kushindwa kumfikia na kuokolewa, Haijalishi mtu ametoka wapi na amefanya nini, Mpango wa Mungu uko pale pale kwamba yeye alikuja duniani kuwaokoa wenye dhambi na kwa sababu hiyo hashindwi kumbadilisha yeyote na kumtumia katika mpango wake mkuu, kimsingi Yesu Kristo ambaye ndiye mwokozi, hakuja duniani kuwaita watu wema bali alikuja kuwaita wenye dhambi na kuokoa wale waliopotea.

Luka 5:30-32 “Ikawa Mafarisayo na waandishi wao kuwanung'unikia wanafunzi wake, wakisema, Mbona mnakula na kunywa pamoja na watoza ushuru na wenye dhambi? Yesu akajibu akawaambia, Wenye afya hawana haja na tabibu, isipokuwa walio hawawezi. Sikuja kuwaita wenye haki, bali wenye dhambi, wapate kutubu.”

Luka 19:9-10 “Yesu akamwambia, Leo wokovu umefika nyumbani humu, kwa sababu huyu naye ni mwana wa Ibrahimu.Kwa kuwa Mwana wa Adamu alikuja kutafuta na kuokoa kile kilichopotea.”

Katika maandiko tunauona moyo wa Mungu, jinsi usivyokuwa na ubaguzi wala mipaka katika kuokoa, Mungu alimuingiza Rahabu yule kahaba katika mpango wake wa ukombozi kwa sababu ya Imani yake kwake, Yeye alimuamini Mungu na kuokolewa, licha ya kuwa na historia mbaya ya maisha ya nyuma, tunajifunza kuwa Mungu anaweza kumuokoa yeyote bila kujali historia ya maisha yake ya nyuma, kama alivyomuokoa Rahabu, Leo tutachukua muda basi kujifunza kwa habari ya Rahabu na kujifunza namna na jinsi ambavyo Mungu anaweza kukuokoa na wewe na kukuingiza katika mpango wake na makusudi yake ya ukombozi bila kujali unatokea wapi.

Tutajifunza ujumbe huu Rahabu yule kahaba kwa kuzingatia mambo ya muhimu yafuatayo!

·         Rahabu alikuwa mtu wa namna gani?

·         Mambo yaliyopelekea maisha ya Rahabu kubadilika

·         Kujifunza kutoka kwa Rahabu yule kahaba


Rahabu alikuwa mtu wa namna gani?

Kwa mujibu wa maandiko Rahabu aliyeishi mwaka wa 1481 Kabla ya Kristo alikuwa ni mwanamke kahaba wa kabila za kikanaani aliyeishi katika jiji la Yeriko, lililokuwako katika inchi ya ahadi, moja ya sifa kubwa inayomtambulisha Rahabu ilikuwa ni pamoja na kazi yake ya ukahaba, Neno Kahaba katika maandiko ya kiebrania linasomeka kama “Zรขnรขh” Neno hilo kwa kiingereza ni Harlot au hookers au zona yaani Prostitute ambalo tafasiri yake ni mtu anayejishughulisha na kuuza mwili wake ili kujipatia fedha, au mtu anayetoa huduma ya tendo la ngono kwa kusudi la kujipatia fedha, Kwa hiyo Rahabu alikuwa ni mtu anayefanya biashara hiyo, sio hivyo tu, Rahabu pia alikuwa anamiliki nyumba ya wageni au nyumba ya kufanyia mapenzi maarufu kama danguro, kwa hiyo ilikuwa rahisi kwa wageni wa kila aina kufikia nyumbani mwake au kwenye nyumba yake ya wageni

Yoshua 2:1-3 “Yoshua, mwana wa Nuni, akawatuma watu wawili kutoka Shitimu kwa siri, ili kupeleleza, akawaambia, Enendeni mkaitazame nchi hii, na Yeriko. Wakaenda wakafika nyumbani kwa kahaba mmoja jina lake aliitwa Rahabu, wakalala huko. Mfalme wa Yeriko akaambiwa, kusema, Tazama, watu wawili wa wana wa Israeli wameingia humu leo usiku, ili kuipeleleza nchi. Mfalme wa Yeriko akatuma watu kwa Rahabu, akasema, Watoe watu wale waliokuja kwako, walioingia ndani ya nyumba yako, maana wamekuja ili kuipeleleza nchi.”

Utafiti wa hivi karibuni unaonyesha kuwa duniani kuna watu wapatao milioni 42 ambao wanajihusisha na biashara ya ukahaba na wengi wao ni wanawake, Ukahaba ni swala lililo kinyume na sheria katika inchi nyingi na linahesabika kama uhalifu, lakini hata hivyo biashara hii inashamiri hata katika maeneo ambayo ni vigumu sana kuamini kuwa yanaweza kuwa na ukahaba, mfano katika nchi ya Jordan ni rahisi kuona waziwazi wanawake wa kiarabu wakijiuza kwa watalii, katika mpango mkakati wa kuhubiri injili, Kanisa halina budi kuwa na Programu maalumu ya kujaribu kusaidia na kuwafikia makahaba au watu wanaojihusisha na biashara hii kwa injili, kwani wengine wamelazimika kuwa hivyo kutokana na kushindwa kuvumilia changamoto mbalimbali za kimaisha, Mungu alimuhurumia Kahaba huyu na kumuokoa na kumsamehe kabisa na kuolewa katika ukoo wa Yuda na hivyo kuingia katika mstari wa wanawake maarufu wanaotajwa katika ukoo wa Masihi

Mathayo 1:1-5 “Kitabu cha ukoo wa Yesu Kristo, mwana wa Daudi, mwana wa Ibrahimu. Ibrahimu alimzaa Isaka; Isaka akamzaa Yakobo; Yakobo akamzaa Yuda na ndugu zake;  Yuda akamzaa Peresi na Zera kwa Tamari; Peresi akamzaa Esromu; Esromu akamzaa Aramu; Aramu akamzaa Aminadabu; Aminadabu akamzaa Nashoni; Nashoni akamzaa Salmoni; Salmoni akamzaa Boazi kwa Rahabu; Boazi akamzaa Obedi kwa Ruthu; Obedi akamzaa Yese; Yese akamzaa mfalme Daudi. Daudi akamzaa Sulemani kwa yule mke wa Uria;”

Mambo yaliyopelekea maisha ya Rahabu kubadilika

Pamoja na changamoto aliyokuwa anakabiliana nayo Rahabu katika maisha yake kama kahaba, Kahaba huyu alikuwa na ufahamu mkubwa au ufahamu mpana jina lake Rahabu katika kiebrania linasomeka kama “Rฤhฤb” au “Rahav” ambalo maana yake mwenye ufahamu mpana au mwenye ufahamu mkubwa, kwa hiyo ni wazi kuwa Rahabu alikuwa ni mwanamke mwenye uelewa mkubwa sana na ufahamu mpana,upana wa ujuzi wake ulihifadhi siri nyingi sana na taarifa kubwa kama bahari. Rahabu alikuwa ni mtu mwenye taarifa nyingi tena zilizo sahihi, kwa hiyo mwanamke huyu vilevile alikuwa “informer” alikuwa ni mtu mwenye uwezo mkubwa wa kudukuu taarifa na ndio maana hata mfalme wa inchi alijua kuwa anaweza kupata taarifa sahihi za wapelekezi walioingia nchini mwake.

Yoshua 2:2-5 “Mfalme wa Yeriko akaambiwa, kusema, Tazama, watu wawili wa wana wa Israeli wameingia humu leo usiku, ili kuipeleleza nchi. Mfalme wa Yeriko akatuma watu kwa Rahabu, akasema, Watoe watu wale waliokuja kwako, walioingia ndani ya nyumba yako, maana wamekuja ili kuipeleleza nchi. Yule mwanamke akawatwaa wale watu wawili, akawaficha, akasema, Naam, wale watu walikuja kwangu, lakini sikujua walikotoka; ikawa kama wakati wa kufungwa lango la mji, kulipokuwa giza, watu wale wakatoka, wala sijui walikokwenda; wafuateni upesi, maana mtawapata.”

Kutokana na uwezo wake mkubwa wa kupata taarifa kahaba huyu alikuwa na taarifa zote za Wana wa Israel na matendo yote ya Mungu wao na alitambua kila kitu kuhusu Wayahudi na Mungu wao Tangu siku walipotoka Misri hivyo alikuwa na taarifa sahihi kuhusu Mungu huyu wa kweli na kuamini

a.       Alimwamini Mungu wa Israel - Yoshua 2:9-11 “ akawaambia wale wanaume, Mimi najua ya kuwa Bwana amewapa ninyi nchi hii, na ya kuwa hofu imetuangukia mbele yenu, na ya kuwa wenyeji wote wa nchi wanayeyuka mbele yenu. Maana tumesikia jinsi Bwana alivyoyakausha maji ya bahari ya Shamu mbele yenu, hapo mlipotoka Misri, tena mambo hayo mliyowatendea wafalme wawili wa Waamori waliokuwa huko ng'ambo ya Yordani, yaani, Sihoni na Ogu, mliowaangamiza kabisa. Na mara tuliposikia hayo mioyo yetu iliyeyuka, wala haukusalia ujasiri wo wote katika mtu awaye yote, kwa sababu yenu; kwa kuwa Bwana, Mungu wenu, yeye ndiye Mungu, katika mbingu juu na katika nchi chini.”

               

b.      Alitaka Agano la ukombozi – Licha ya kuwa na taarifa nyingi na sahihi na pana kuhusu Waisrael na kuhusu Mungu wao, Rahabu pia alijua ni namna gani anaweza kuyaokoa maisha yake na familia yake, alitambua namna anavyoweza kujiepusha na maangamizi kwa sababu hiyo alifahamu namna na jinsi anavyoweza kujiweka salama kwa kuingia katika agano na Mungu wa Israel na watu wake kwa sababu hiyo aliwaomba wapelelezi wamuhakikishie wokovu wake na nyumba yote ya baba yake

 

Yosua 2:12-14 “Basi sasa, nawasihi, niapieni kwa Bwana, kwa kuwa nimewatendea ihisani, ya kwamba ninyi nanyi mtaitendea ihisani nyumba ya baba yangu; tena nipeni alama ya uaminifu; ya kwamba mtawaponya hai baba yangu na mama yangu, na ndugu zangu wanaume na wanawake, na vitu vyote walivyo navyo, na kutuokoa roho zetu na kufa. Wale wanaume wakamwambia, Uhai wetu badala ya uhai wenu, ikiwa hamwitangazi habari ya shughuli yetu hii; kisha itakuwa, wakati Bwana atakapotupa nchi hii, tutakutendea kwa ihisani na uaminifu.”

 

c.       Alionyesha Imani na matendo – Licha ya kumuamini Mungu wa Israel Rahabu aliwatendea mema wapelelezi wale kwa kuwaficha  na kuwaelekeza njia ya kutorokea aliwalinda na hakutaka kuwatoa kwa watu wanchi yake ili wauawe au kukamatwa, aliwatendea mema watu wa Mungu

 

Yoshua 2:15-16 “Ndipo akawashusha kwa kamba dirishani, maana nyumba yake ilikuwa katika ukuta wa mji; naye alikaa ukutani. Akawaambia, Enendeni zenu mlimani, wale wanaowafuatia wasije wakawapata; mkajifiche huko siku tatu hata wao wanaowafuatia watakaporudi; kisha enendeni zenu.           

 

Yakobo 2:25 “Vivyo hivyo na Rahabu, yule kahaba naye, je! Hakuhesabiwa kuwa ana haki kwa matendo, hapo alipowakaribisha wajumbe, akawatoa nje kwa njia nyingine? Maana kama vile mwili pasipo roho umekufa, vivyo hivyo na imani pasipo matendo imekufa.”         

Kujifunza kutoka kwa Rahabu yule kahaba

Ni wazi kuwa mtu huyu hakuwa myahudi wala hakuwa mwenye metendo mema alikuwa kahaba, lakini Mungu alimuokoa kwa sababu alimuamini Mungu, Yesu Kristo amekuja duniani sio kwaajili ya watu Fulani maalumu, Mungu yuko tayari kumuokoa mtu yeyote wa kabila lolote na wa historia yoyote maadamu tu mtu huyo atamuamini Mungu aliye hai na kazi yake ya ukombozi kupitia mwanae mpendwa Yesu Kristo

Yohana 3:16 -18 “Kwa maana jinsi hii Mungu aliupenda ulimwengu, hata akamtoa Mwanawe pekee, ili kila mtu amwaminiye asipotee, bali awe na uzima wa milele. Maana Mungu hakumtuma Mwana ulimwenguni ili auhukumu ulimwengu, bali ulimwengu uokolewe katika yeye. Amwaminiye yeye hahukumiwi; asiyeamini amekwisha kuhukumiwa; kwa sababu hakuliamini jina la Mwana pekee wa Mungu.”

Awaye yote akimuamini Yesu Kristo, ataokolewa bila kujali kuwa anatokea katika historia gani, wala Mungu haangalii makosa yetu ya zamani na badala yake anatazama moyo uliobadilika kumuelekea yeye, Mungu alimuinua Kahaba Rahabu na kumpeleka juu sana hata kuwa sehemu ya ukoo wa Yesu Kristo, wakati mwingine kuonelewa kwako sana na ibilisi kunadhihirisha wivu mkubwa sana alio nao kwako endapo Mungu angekutana na wewe

Wokovu na haki ya Mungu sio vitu vinavyopatikana kwa jitihada na matendo ya kibinadamu, bali Imani katika Mungu na neema anayoitoa yeye, neema hii inaweza kwenda kwa yeyote yule bila kujali historia yake.

Waefeso 2:8-9. “Kwa maana mmeokolewa kwa neema, kwa njia ya imani; ambayo hiyo haikutokana na nafsi zenu, ni kipawa cha Mungu; wala si kwa matendo, mtu awaye yote asije akajisifu.”

No one is too special to meet the Grace of God, Hakuna mtu ambaye yeye anaweza kudai kuwa ni maalumu sana mpaka aweze kupokea neema ya Mungu, ni Imani yako kwake tu ndiyo inayoweza kumgusa na akabadilisha maisha yako, huna lolote unaloweza kulifanya ukampendeza yeye, zaidi ya kuamini. Usihuzunike kwa sababu labda umewahi kupitia historia mbaya zaidi ya maisha yasiyofaa ambayo labda unaweza kudhania kuwa kwajili ya hayo hustahili kuhurumiwa na Mungu, lakini nakutangazia kuwa haijalishi umepitia maisha mabaya kiasi gani, Rahabu ni ishara ya kuwa hata wewe unaweza kupokelewa na Mungu na historia ya maisha yako ikabadilika, ukamtangaza Kristo.

2Wakorintho 5:17 “Hata imekuwa, mtu akiwa ndani ya Kristo amekuwa kiumbe kipya; ya kale yamepita tazama! Yamekuwa mapya.”

Yeriko ulipoharibiwa Rahabu pamoja na familia yake na nyumba ya baba yake waliokolewa wote kwa sababu ya Imani na agano lile aliloapiwa na Wapelelezi katika inchi ya Kanaani, Mungu alikuwa mwaminifu kwa ahadi zake, na watu wake walikuwa wamejifunza kusimamia viapo vyao kwani Yoshua alikumbuka kuwa yuko mtu ambaye hastahili kuangamizwa kwa sababu amemuamini Mungu wa Israel na ana agano na Mungu wa Yakobo!

Yoshua 6:22-25 “Naye Yoshua akawaambia wale wanaume wawili walioipeleleza nchi, Ingieni katika nyumba ya yule kahaba, mkamtoe huyo mwanamke mwenyewe na vitu vyote alivyo navyo, kama mlivyomwapia. Basi wale vijana wapelelezi wakaingia, wakamtoa Rahabu, na baba yake, na mama yake, na ndugu zake, na vitu vyote walivyokuwa navyo, wakawatoa na jamaa zake wote pia; wakawaweka nje ya matuo ya Israeli. Kisha wakauteketeza mji kwa moto, na vitu vyote vilivyokuwa ndani yake; bali fedha, na dhahabu, na vyombo vya shaba, na vya chuma, wakavitia katika hazina ya nyumba ya Bwana. Lakini Yoshua akamhifadhi Rahabu, yule kahaba, na watu wa nyumba ya baba yake, na vitu vyote alivyokuwa navyo; naye akakaa kati ya Israeli hata leo; kwa sababu aliwaficha wale wajumbe aliowatuma Yoshua ili kuupeleleza mji wa Yeriko.”     

Wokovu ni zawadi ya Mungu kwa watu wote, Mungu hana upendeleo, hatupaswi kujivunia wokovu na kujifikiri kuwa sisi ni watu maalumu sana kuliko wengine, Mungu ni Mungu wa wote wenye mwili anaweza kumuokoa yeyote na anaweza kumuinua yeyote ana anaweza kumtumia yeyote, wapelelezi hawakuweza kabisa kumdharau Rahabu kwa sababu ya ukahaba wake na maisha yake yaliyopita badala yake walimuheshimu na kumsikiliza, na walifuata maelekezo yake. Mungu alimhamisha Rahabu kutoka katika maisha ya dhambi kwenda katika historia ya ukombozi wa mwanadamu, ni kupitia rehema za Mungu, na neema yake yeye anaweza kuwafikiwa watu wote na wa jinsia zote na imani zote duniani, hupaswi kujikinai na kujifikiri kuwa wewe ni mtu asiyefaa, badala yake mtazame yule tu awezaye kuokoa, haki yetu haihesabiwi na wanadamu, haki yetu inahesabiwa na Mungu na hakuna mwanadamu yeyote mwenye mamlaka ya kutushitaki

Zaburi 130:3-4 “Bwana, kama Wewe ungehesabu maovu, Ee Bwana, nani angesimama? Lakini kwako kuna msamaha, Ili Wewe uogopwe.”

Warumi 8:33-34 “Ni nani atakayewashitaki wateule wa Mungu? Mungu ndiye mwenye kuwahesabia haki. Ni nani atakayewahukumia adhabu? Kristo Yesu ndiye aliyekufa; naam, na zaidi ya hayo, amefufuka katika wafu, naye yuko mkono wa kuume wa Mungu; tena ndiye anayetuombea.”        

Na. Rev. Innocent Mkombozi bin Samuel bin Hamza bin Jumaa bin Athumani bin Salim Kamote

Mkuu wa wajenzi mwenye hekima!

Jumapili, 22 Juni 2025

Malkia wa Sheba atasimama na watu wa kizazi hiki!


Mathayo 12:42 “Malkia wa kusini atasimama siku ya hukumu pamoja na watu wa kizazi hiki, naye atawahukumu kuwa wamekosa; kwa sababu yeye alikuja kutoka pande za mwisho za dunia ili asikie hekima ya Sulemani, na hapa yupo aliye mkuu kuliko Sulemani.”




Utangulizi:

Moja ya wanawake maarufu katika Biblia ni pamoja na Malkia wa kusini (Malkia wa Sheba) Mwanamke huyu mashuhuri mwenye mikogo isiyokuwa ya kawaida amewahi kusifiwa na Yesu Kristo kama moja ya mwanadamu mwenye maamuzi thabiti ya kutafuta hekima kwa gharama yoyote ile bila kujali umbali, Mwanamke huyu alikataa ujinga na kuona kuliko kubaki na ujinga ni vema akasafiri kwenda mbali kwa gharama kubwa kwenda kuitafuta Hekima, Aliandaa maswali yake magumu na akasafiri mpaka Yerusalem makao makuu ya mji wa Israel kwaajili ya kusikia na kupokea Hekima kutoka kwa mfalme Suleimani, Hekima ambayo Suleimani alipewa na Mungu.

1Wafalme 10:1-13 “Na malkia wa Sheba aliposikia habari za Sulemani juu ya jina la Bwana, alikuja ili amjaribu kwa maswali ya fumbo. Akaingia Yerusalemu na wafuasi wengi sana, na ngamia wachukuao manukato, na dhahabu nyingi sana, na vito vya thamani; alipomfikilia Sulemani, akazungumza naye mambo yote aliyokuwa nayo moyoni. Naye Sulemani akamfumbulia maswali yake yote; wala hakukuwa na neno alilofichiwa mfalme asimwambie. Naye malkia wa Sheba alipoona hekima yote ya Sulemani, na nyumba aliyokuwa ameijenga, na chakula cha mezani pake, na watumishi wake walivyokaa, na kusimamia kwao wangoje wake, na mavazi yao, na wanyweshaji wake, na daraja yake ya kupandia mpaka nyumba ya Bwana, roho yake ilizimia. Akamwambia mfalme, Ndizo kweli habari zile nilizozisikia katika nchi yangu za mambo yako na za hekima yako. Lakini mimi sikuzisadiki habari hizo, hata nilipokuja na kuona kwa macho yangu; tena, tazama, sikuambiwa nusu; wewe umezidi kwa hekima na kufanikiwa kuliko habari nilizozisikia. Heri watu wako, na heri watumishi hawa wako, wasimamao mbele yako siku zote, wakisikia hekima yako. Na ahimidiwe Bwana, Mungu wako, aliyependezwa nawe, ili akuweke juu ya kiti cha enzi cha Israeli; kwa kuwa Bwana amewapenda Israeli milele, kwa hiyo amekufanya kuwa mfalme, ufanye hukumu na haki. Basi akampa mfalme talanta za dhahabu mia na ishirini, na manukato mengi, mengi sana, na vito vya thamani; wala haukuja tena wingi wa manukato, kama hayo malkia wa Sheba aliyompa mfalme Sulemani. Tena merikebu za Hiramu, zilizochukua dhahabu kutoka Ofiri, zikaleta kutoka Ofiri miti ya msandali mingi sana, na vito vya thamani. Mfalme akafanya kwa mia hiyo ya msandali nguzo za nyumba ya Bwana, na za nyumba ya mfalme, na vinubi na vinanda vya hao waimbaji; wala haikuja miti ya msandali kama hiyo, wala haikuonekana, hata leo. Naye mfalme Sulemani akampa malkia wa Sheba haja yake yote, kila alilotaka, zaidi ya hayo aliyopewa na Sulemani kwa ukarimu wake wa kifalme. Basi, akarudi akaenda zake katika nchi yake, yeye na watumishi wake.”

Leo basi tutachukua muda kujifunza kwa habari ya mwanamke huyu mashuhuri katika Biblia ili tuweze kujifunza na kufuata mfano wake wa kutafiti na kutafuta kujua habari za Yesu Kristo ambaye ni mkuu kuliko Suleimani kwa gharama yoyote, Ikiwa yeye alitoka pande za mwisho za dunia kwaajili ya kutafuta Hekima kwa Suleimani sisi kama watu wa Mungu tunajikumbusha kuitafuta hekima ya Yesu Kristo, tutajifunza somo hili Malkia wa Sheba atasimama na watu wa kizazi hiki kwa kuzingatia vipengele vitatu vifuatavyo:-


·         Ufahamu kuhusu malkia wa Sheba.

·         Kujifunza kutoka kwa malkia wa Sheba.

·         Malkia wa sheba atasimama na watu wa kizazi hiki.


Ufahamu kuhusu malkia wa Sheba.

Malkia wa Sheba ni moja ya wanawake maarufu sana katika Biblia, mwanamke huyu alitawala katika eneo la Pembe ya Afrika hususani Ethiopia na sehemu za Asia ya kusini yaani uarabuni au Arabuni ya kusini, wakazi wa eneo lake waliitwa Sheba au Saba, eneo la utawala wake ulikuwa ni sehemu ya Uarabuni ya kusini na pembe ya Afrika ikijumuisha mataifa ya Yemen, Eritrea, Sudani, na Ethiopia, Malkia huyu ni maarufu kwa jina la “Bilqis” katika lugha ya kiarabu akiwa maarufu sana huko Yemen kwa jina hilo, na pia akijulikana kwa jina la “Makeda” katika nchi ya Ethiopia, hata hivyo Malikia huyu hakutajwa kwa jina lake katika Neno la Mungu yaani Biblia, lakini anatajwa tu kama Malikia wa kusini au Sheba au “Malkat Saba” kwa kiebrania na kwa kirumi “Basilissa Saba” katika Biblia ya Septuagint. Habari zake na kuvuma kwake katika historia amekuwa maarufu zaidi katika Taifa la Ethiopia zaidi kuliko Yemen ambao kila mmoja anadai ndiko alikotokea Malkia huyu, hata hivyo tafiti zinaonyesha kuwa waseba au washeba waliishi eneo lote la uarabuni na pembe ya Afrika kwa hiyo huenda utawala wake ulikuwa ni eneo lote la pembe ya Afrika na maeneo ya Arabuni ya kusini, Yemen na Oman yaani arabuni ya kusini ya leo. Lakini anatajwa zaidi katika eneo la Ethiopia ambako watoto wake walitawala badala yake, historia za kale za Kiethiopia  ziitwazo Kebra Negast zinaonyesha kuwa alitembelea Yerusalem na alizaa mtoto na Mfalme Suleimani na mtoto huyu aliitwa Meneleki I ambaye alikuwa baba wa wafalme wote wa Ethiopia wenye nasaba na mfalme Suleimani huko Ethiopia mpaka Mfalme maarufu zaidi Haile Selassie.  Malkia wa Sheba Anajitokeza katika maandiko akisafiri kwa ngamia, akiwa na zawadi ya viungo mbalimbali, dhahabu na mawe ya thamani akisafiri kwa safari ya msafara wa kifahari mpaka kwa Suleimani kwaajili ya kujifunza na kuuliza maswali magumu ya maisha kutoka kwake, vyovyote ilivyo Malkia huyu ana jambo muhimu la kutufunza ambalo ni kubwa kuitafuta Hekima pamoja na mambo mengine.

1Wafalme 10:1-10 “Na malkia wa Sheba aliposikia habari za Sulemani juu ya jina la Bwana, alikuja ili amjaribu kwa maswali ya fumbo. Akaingia Yerusalemu na wafuasi wengi sana, na ngamia wachukuao manukato, na dhahabu nyingi sana, na vito vya thamani; alipomfikilia Sulemani, akazungumza naye mambo yote aliyokuwa nayo moyoni. Naye Sulemani akamfumbulia maswali yake yote; wala hakukuwa na neno alilofichiwa mfalme asimwambie. Naye malkia wa Sheba alipoona hekima yote ya Sulemani, na nyumba aliyokuwa ameijenga, na chakula cha mezani pake, na watumishi wake walivyokaa, na kusimamia kwao wangoje wake, na mavazi yao, na wanyweshaji wake, na daraja yake ya kupandia mpaka nyumba ya Bwana, roho yake ilizimia. Akamwambia mfalme, Ndizo kweli habari zile nilizozisikia katika nchi yangu za mambo yako na za hekima yako. Lakini mimi sikuzisadiki habari hizo, hata nilipokuja na kuona kwa macho yangu; tena, tazama, sikuambiwa nusu; wewe umezidi kwa hekima na kufanikiwa kuliko habari nilizozisikia. Heri watu wako, na heri watumishi hawa wako, wasimamao mbele yako siku zote, wakisikia hekima yako. Na ahimidiwe Bwana, Mungu wako, aliyependezwa nawe, ili akuweke juu ya kiti cha enzi cha Israeli; kwa kuwa Bwana amewapenda Israeli milele, kwa hiyo amekufanya kuwa mfalme, ufanye hukumu na haki. Basi akampa mfalme talanta za dhahabu mia na ishirini, na manukato mengi, mengi sana, na vito vya thamani; wala haukuja tena wingi wa manukato, kama hayo malkia wa Sheba aliyompa mfalme Sulemani.”

Maandiko yanamtaja mwanamke huyu kwa sifa kubwa tano muhimu sana:-


1.       Alikuwa Mtafiti, mwenye kupenda kujifunza na mwenye busara.

 

Malikia huyu anasifiwa katika maandiko kama mwanamke ambaye licha ya kuwa kiongozi katika taifa lake yeye aliposikia habari za Hekima ya mfalme Suleimani, akapanga kusafiri kutoka nchi ya mbali, Yesu anaita pande za mwisho wa Dunia kwaajili ya kujifunza kutoka kwa Mfalme huyu mwenye hekima na tunaelezwa kuwa alikuwa amejipanga kwani alikuja na maswali magumu sana kwa Mfalme Suleimani ambayo alijibiwa yote na roho yake ikazimia. Napenda sana tafasiri ya kiingereza ya NIV inaeleza hivi “She came to Jerusalem to test him with hard questions” yaani malikia huyu alikuja Yerusalem kumjaribu (Suleimani) kwa Maswali magumu sana na maswali yake yote yalijibiwa.

 

2Nyakati 9:1-9 “Na malkia wa Sheba aliposikia habari za Sulemani, alikuja ili amjaribu Sulemani kwa maswali ya fumbo huko Yerusalemu, mwenye wafuasi wengi, na ngamia wachukuao manukato, na dhahabu nyingi sana, na vito vya thamani; alipomfikilia Sulemani, akamwambia mambo yote aliyokuwa nayo moyoni mwake. Naye Sulemani akamfumbulia maswali yake yote; wala halikuwako neno alilofichiwa Sulemani, asimwambie. Naye malkia wa Sheba alipoona hekima ya Sulemani, na nyumba aliyoijenga, na vyakula vya mezani mwake, na kikao cha watumishi wake, na usimamizi wao wangoje wake, na mavazi yao; na wanyweshaji wake, na mavazi yao; na daraja yake ya kupandia mpaka nyumba ya Bwana; roho yake ilizimia. Akamwambia mfalme, Ndizo kweli habari zile nilizozisikia katika nchi yangu za mambo yako na za hekima yako. Lakini mimi sikuyasadiki maneno yao, hata nilipokuja na kuona kwa macho yangu; wala, tazama, ukuu wa hekima yako sikuambiwa nusu; wewe umezidi kuliko habari nilizozisikia. Heri watu wako, na heri hawa watumishi wako, wasimamao mbele yako sikuzote, wakisikia hekima yako. Na ahimidiwe Bwana, Mungu wako, aliyependezwa nawe, ili akuweke juu ya kiti chake cha enzi, kuwa mfalme wake Bwana, Mungu wako; kwa kuwa Mungu wako amewapenda Israeli, kuwathibitisha milele, kwa hiyo amekufanya kuwa mfalme juu yao, ufanye hukumu na haki. Basi akampa mfalme talanta mia na ishirini za dhahabu, na manukato mengi mengi sana, na vito vya thamani; wala haukuja wingi wa manukato, kama hayo aliyopewa mfalme Sulemani na malkia wa Sheba.”

 

2.        Alikuwa mkarimu mtoaji:

 

Maandiko yamenukuu zawadi alizokuja nazo Malkia wa Sheba kwa  Mfalme Suleimani kuwa ni zawadi za kipekee na nyingi sana kiasi kwamba neno la Mungu linasema kuwa wala hakujawahi kuja tena wingi wa manukato sawa na yale ambayo malkia wa Sheba aliwahi kumletea Suleimani, utoaji huu unatufunza ya kuwa Malkia huyu alikuwa na moyo wa utoaji alikuwa na moyo wa ukarimu, hakutaka kumtembelea mtumishi wa Mungu, huku akiwa mikono Mitupu, alitambua ya kuwa kutokana na umaarufu aliokuwa nao Suleimani na utajiri wake hangehitaji kitu lakini Moyo wa malikia unaonekana tena katika eneo hili, wote tunajua kuwa Mungu ambaye ni mfalme wetu ana kila kitu na hahitaji lolote kutoka kwetu lakini Moyo wetu wa ukarimu kwake unaweza kupelekea yeye aturidhie, na kuipokea sadaka yetu kama alivyofanya Habili. Suleimani aliipokea zawadi na kumpa zawadi mara dufu kuliko zake

 

1Wafalme 10:13 “Basi akampa mfalme talanta za dhahabu mia na ishirini, na manukato mengi, mengi sana, na vito vya thamani; wala haukuja tena wingi wa manukato, kama hayo malkia wa Sheba aliyompa mfalme Sulemani. Tena merikebu za Hiramu, zilizochukua dhahabu kutoka Ofiri, zikaleta kutoka Ofiri miti ya msandali mingi sana, na vito vya thamani. Mfalme akafanya kwa mia hiyo ya msandali nguzo za nyumba ya Bwana, na za nyumba ya mfalme, na vinubi na vinanda vya hao waimbaji; wala haikuja miti ya msandali kama hiyo, wala haikuonekana, hata leo. Naye mfalme Sulemani akampa malkia wa Sheba haja yake yote, kila alilotaka, zaidi ya hayo aliyopewa na Sulemani kwa ukarimu wake wa kifalme. Basi, akarudi akaenda zake katika nchi yake, yeye na watumishi wake.”

 

3.       Alikuwa mwenye bidii kuitafuta hekima.

 

Malikia huyu anasifiwa na Yesu Kristo kuwa alitoka pande za mwisho za dunia yaani katika ncha ya bara la Afrika kutoka mbali sana Ethiopia na kuja kuitafiti Hekima ya Suleimani, Yesu anasema Malikia huyu atasimama siku ya hukumu na watu wa kizazi hiki kuwahukumu kwa uzembe, kukosa bidii, moyo wa kujifunza wakati wao wamejaaliwa sana Hekima iliyokubwa kuliko ya Sulemaini, yaani mafundisho ya Yesu Kristo!

 

Mathayo 12:42 “Malkia wa kusini atasimama siku ya hukumu pamoja na watu wa kizazi hiki, naye atawahukumu kuwa wamekosa; kwa sababu yeye alikuja kutoka pande za mwisho za dunia ili asikie hekima ya Sulemani, na hapa yupo aliye mkuu kuliko Sulemani.”

 

Maandiko yanatuasa kuitafuta hekima kwa gharama yoyote ile, kutokana na hekima kuwa na thamani kuliko madini yoyote Malikia huyu aliigundua siri hiyo na kujitajidi sana kuitafuta Hekima, alikuwa na bidii katika kutaka kufahamu na kujifunza tofauti sana na watu wa kizazi hiki, kama yeye alisafiri kwenda mbali sana kutafuta maarifa akiwa na maswali yake magumu je watu wa kizazi hiki unaweza kuwaandalia kila kitu lakini wakawa wavivu wa kusoma tu! Nyakati za leo hekima inapatikana karibu sana, Elimu na ujuzi na maarifa yako katika kiganja cha kila mtu leo, lakini watu hawana hamu wala kiu na shauku ya kujipa muda wa kusoma na kujifunza n ahata kufanya utafiti wa neno la Mungu tu, na unapoandaa mada na ikawa ndefu kwaajili ya kuweka mafafanuzi zaidi kizazi hiki hakitaki, kinafurahia kuperuzi, habari za udaku, koneksheni, siasa, michezo na burudani lakini kiu ya hekima ya kiungu na kuutafuta uso wa Mungu imekuwa ni ndogo sana, malikia anatufundisha kuyatafuta maarifa.

 

Mithali 4:5-7 “Jipatie hekima, jipatie ufahamu; usiusahau; Wala usiyakatae maneno ya kinywa changu. Usimwache, naye atakuhifadhi; Umpende, naye atakulinda. Bora hekima, basi jipatie hekima; Naam, kwa mapato yako yote jipatie ufahamu.”

 

4.       Alikuwa mcha Mungu.

 

Katika lugha yake kumhusu Suleimani malikia huyu anaonyesha ya kuwa alikuwa na ujuzi kuhusu Mungu na alikuwa mcha Mungu, Yeye hakuwa tu amevutiwa na Suleimani pekee bali alikuwa amesikia habari za Mungu wa Suleimani, maandiko yanaonyesha kuwa ni kwaajili ya jina la Bwana alikuja na sio hivyo tu bali pia alimtukuza Mungu wa Suleimani kutokana na umaminifu wake kwake na kwa watu wake Israel.  Na alitambua kuwa Mungu anawapenda Wayahudi.

 

1Wafalme 10:1 “Na malkia wa SHEBA ALIPOSIKIA HABARI ZA SULEMANI JUU YA JINA LA BWANA, alikuja ili amjaribu kwa maswali ya fumbo.”

 

2Nyakati 9:5-8 “Akamwambia mfalme, Ndizo kweli habari zile nilizozisikia katika nchi yangu za mambo yako na za hekima yako. Lakini mimi sikuyasadiki maneno yao, hata nilipokuja na kuona kwa macho yangu; wala, tazama, ukuu wa hekima yako sikuambiwa nusu; wewe umezidi kuliko habari nilizozisikia. Heri watu wako, na heri hawa watumishi wako, wasimamao mbele yako sikuzote, wakisikia hekima yako. NA AHIMIDIWE BWANA, MUNGU WAKO, aliyependezwa nawe, ili akuweke juu ya kiti chake cha enzi, kuwa mfalme wake Bwana, Mungu wako; kwa kuwa Mungu wako amewapenda Israeli, kuwathibitisha milele, kwa hiyo amekufanya kuwa mfalme juu yao, ufanye hukumu na haki.”           

 

5.       Alitambua kuwa Mungu anawapenda Israel.

 

Malikia huyu alipoona kuwa Mungu amewapa watu wake Israel kiongozi mzuri, mwenye hekima ya kupita kawaida alielewa wazi kuwa hukumu na haki zitafanyika vizuri, maamuzi mazuri ya kumpendeza Mungu yatafanyika kwa manufaa ya taifa la Israel, alielewa wazi kuwa Mungu anawapenda Israel, Mungu akilipenda taifa lolote lile atalisimamishia kiongozi mzuri, Mcha Mungu na mwenye kuchukia rushwa na mwenye kupenda haki na asiye na upendeleo ambaye ataamua mambo kwa haki, Lakini Mungu akitaka kuwahukumu ataachilia kiongozi mbaya awatawale, siri ya mafanikio ya taifa lolote lile kuinuka ni pamoja na taifa hilo kuwa taifa la haki.

 

Mithali 14:34 “Haki huinua taifa; Bali dhambi ni aibu ya watu wo wote.” Mithali 29:2 “Wenye haki wakiwa na amri, watu hufurahi; Bali mwovu atawalapo, watu huugua.”

 

Uwepo wa kiongozi kama Suleimani mwenye akili nyingi na hekima nyingi kulimfanya malikia wa Sheba kutafasiri kuwa Mungu anawapenda watu wake Israel, Kama Malikia wa Sheba angepata nafasi ya kumuona Bwana Yesu akiwa duniani angelisema Mungu ameupenda ulimwengu, kwa kuwa Yesu ni mkuu kuliko Suleimani. Na maamuzi yake na utawala wake ni wa haki

 

Kujifunza kutoka kwa malkia wa Sheba

Umuhimu wa kufanya utafiti – Malikia wa Sheba hakukubali kusikia tu kuhusu Suleimani bali yeye mwenyewe alitaka kuthibitisha na kujipatia ukweli wa Mambo na kuona kama ndivyo ulivyo, wakristo tunajifunza hapa umuhimu wa kufanya utafiti, unaposikia jambo, au mafundisho ya injili hata kama yanatolewa na muhubiri mkubwa kiasi gani ni lazima kufanya utafiti na kujiridhisha ili uone kama mambo ndivyo yalivyo, Utafiti unasaidia kujua mzizi wa jambo lolote iwe ni tukio, fundisho, majungu, masingizio na kadhalika na kutusaidia kupata suluhu ya mambo, Utafiti wa kina unatusaidia kujithibitishia mambo, kupata ushahidi, kujifunza, kupata taarifa, kudhibiti matukio na kadhalika, utafiti unasaidia kujenga usalama wa taifa, Malikia alikuwa na taarifa za kila kinachoendelea ulimwenguni, na sasa alitaka kujionea ukweli wa mambo na kujithibitishia kama hakuna chumvi katika hilo na kupata kweli iliyonyooka

1Wafalme 10:6-7 “Akamwambia mfalme, Ndizo kweli habari zile nilizozisikia katika nchi yangu za mambo yako na za hekima yako. LAKINI MIMI SIKUZISADIKI HABARI HIZO, HATA NILIPOKUJA NA KUONA KWA MACHO YANGU; tena, tazama, sikuambiwa nusu; wewe umezidi kwa hekima na kufanikiwa kuliko habari nilizozisikia.”          

Kwa bahati mbaya sana wakristo wa nyakati za leo hawana muda wa kufanya utafiti kuhusu neno la Mungu na mambo mengine na kujithibitiashia kama neno hilo ndivyo lilivyo na kwa sababu hiyo watu wengi leo ni rahisi kudanganyika, kumekuwa na mafundisho mengi potofu katika nyakati za leo, au mafundisho ambayo hayako sawa na kweli za neno la Mungu aidha kwa sababu ya watu wenye hila au kwa sababu ya kutafasiriwa vibaya kwa neno la Mungu bila nia ovu, hata hivyo jambo la kusikitisha ni kuwa watu wengi wa kizazi hiki wamekosa uungwana kwani hawayachunguzi mambo ili kupata uhakika wake Malikia anatufundisha kuwa ni lazima tufanye uchunguzi na utafiti, tusikimbilie haraka hara kuamini kila tunachofundishwa na kuitikia amina lakini tufanye utafiti, tujithibitishie wenyewe, na ikiwezekana kujionea wenyewe!

Matendo 17:10-11 “Mara hao ndugu wakawapeleka Paulo na Sila usiku hata Beroya. Nao walipofika huko wakaingia katika sinagogi la Wayahudi. Watu hawa walikuwa waungwana kuliko wale wa Thesalonike, kwa kuwa walilipokea lile neno kwa uelekevu wa moyo, wakayachunguza maandiko kila siku, waone kwamba mambo hayo ndivyo yalivyo.”

Je wewe huwa unafanya utafiti wa mambo na kujiridhisha kama ndivyo yalivyo? Ukifanya hivyo utakuwa na busara kama Malikia wa Sheba na watu wa Beroya, Yesu alipoagiza wakristo wawe wanafunzi hakutaka tuwe tu watu waamini bali alitaka tuwe shule tujifunze, tuwe na maswali yetu na tutafute namna ya kujibizana, tufanye utafiti na kujithibitishia mambo.Kila kitu duniani kinahitaji utafiti lakini Neno la Mungu linahitaji utafiti zaidi kwa ubora wake na viwango vyake

Uthubutu wa kufanya mambo makubwa – Malikia wa Sheba alithubutu kusafiri safari ndefu sana kwaajili ya kutafuta maarifa na Elimu, Lakini pia kwaajili ya jina la Mungu na kwaajili ya kuitafuta kweli, Neno uthubutu katika kiyunani ni “AfthentikฯŒtita” kwa kiingereza “Authenticity” maana yake ni kanuni ya kujithibitishia, kujihakikishia, kutaka kujionea, kutaka kuweka mambo sawasawa, Mtu anayetafuta hekima na maarifa anataka kuweka mambo sawa, Malikia alithubutu, tunaagizwa katika maandiko kuitafuta sana na kuishika sana Elimu, hekima na maarifa na kuwa na bidii hata kuthubutu kufanya lolote tukitafuta mambo makubwa kwaajili ya Mungu. Malkia alisafiri kutoka mbali sana huu ni uthubutu, wa kufanya mambo makubwa kwaajili ya utukufu wa Mungu na ndio uthubutu uliosifiwa na Bwana Yesu Je wewe unathubutu?

Mathayo 12:42 “Malkia wa kusini atasimama siku ya hukumu pamoja na watu wa kizazi hiki, naye atawahukumu kuwa wamekosa; kwa sababu yeye alikuja kutoka pande za mwisho za dunia ili asikie hekima ya Sulemani, na hapa yupo aliye mkuu kuliko Sulemani.”

Alikuwa mkarimu – Maandiko yanatufundisha kuwa wakarimu, kanuni mojawapo ya mafanikio ya kibiblia ni kutoa au kuwapa watu vitu, na tunapofanya hivyo Mungu hutubariki zaidi, hakuna kanuni ya kumpangia mtu katika utoaji msingi wa agano jipya unawataka watu kutoa kwa ukarimu, au kwa kadiri ya neema waliyojaliwa na Bwana, kwa hiyari na kwa moyo mkunjufu, utoaji na ukarimu ni sehemu muhimu sana ya kuonyesha ubora wa mtu! Upendo wake na kujitoa kwake.

Matendo 20:34-35 “Ninyi wenyewe mnajua ya kuwa mikono yangu hii imetumika kwa mahitaji yangu na ya wale waliokuwa pamoja nami. Katika mambo yote nimewaonyesha ya kuwa kwa kushika kazi hivi imewapasa kuwasaidia wanyonge, na kuyakumbuka maneno ya Bwana Yesu, jinsi alivyosema mwenyewe, Ni heri kutoa kuliko kupokea.”

Luka 6:38 “Wapeni watu vitu, nanyi mtapewa; kipimo cha kujaa na kushindiliwa, na kusukwa-sukwa hata kumwagika, ndicho watu watakachowapa vifuani mwenu. Kwa kuwa kipimo kile kile mpimacho ndicho mtakachopimiwa.”

Ni ukweli ulio wazi kuwa kanuni hii ya mafundisho ya Bwana Yesu ilifanya kazi kwa Malikia wa Kushi, kwani ni ukweli usiopingika kuwa wakati anajitoa na zawadi nyingi sana kwa mfalme Suleimani, Mfalme alimpa yeye zawadi zilizo nyingi zaidi kuliko alizotoa yeye, na kututhibitishia ukweli wa lile neno apandaye kwa ukarimu atavuna kwa ukarimu

2Nyakati 9:9-12 “Basi akampa mfalme talanta mia na ishirini za dhahabu, na manukato mengi mengi sana, na vito vya thamani; wala haukuja wingi wa manukato, kama hayo aliyopewa mfalme Sulemani na malkia wa Sheba. Tena watumishi wa Hiramu, pamoja na watumishi wa Sulemani, walioleta dhahabu kutoka Ofiri, wakaleta miti ya msandali, na vito vya thamani. Mfalme akayafanya kwa miti hiyo ya msandali madari ya nyumba ya Bwana, na nyumba ya mfalme, na vinubi na vinanda vya hao waimbaji; wala haijatokea kama hiyo katika nchi ya Yuda. Mfalme Sulemani akampa malkia wa Sheba haja yake yote, kila alilotaka, zaidi ya vile alivyomletea mfalme. Basi akarudi, akaenda zake katika nchi yake, yeye na watumishi wake.”

2Wakorintho 9:6-7 “Lakini nasema neno hili, Apandaye haba atavuna haba; apandaye kwa ukarimu atavuna kwa ukarimu. Kila mtu na atende kama alivyokusudia moyoni mwake, si kwa huzuni, wala si kwa lazima; maana Mungu humpenda yeye atoaye kwa moyo wa ukunjufu.”                                             

Alimwabudu Mungu wa Israel – Malikia wa Sheba alimuabudu Mungu wa Israel, yeye alitambua wazi kuwa Mungu amempa Suleimani ile hekima kwaajili ya utukufu wake na kwaajili ya upendo kwa watu wake hivyo baada ya kujithibitishia ukweli wa Mambo alimuabudu Mungu wa Israel na kumhimidi. Hakuna jambo muhimu na kubwa sana duniani kuliko yote kama kumuabudu Mungu.

2Nyakati 9:5-8 “Akamwambia mfalme, Ndizo kweli habari zile nilizozisikia katika nchi yangu za mambo yako na za hekima yako. Lakini mimi sikuyasadiki maneno yao, hata nilipokuja na kuona kwa macho yangu; wala, tazama, ukuu wa hekima yako sikuambiwa nusu; wewe umezidi kuliko habari nilizozisikia. Heri watu wako, na heri hawa watumishi wako, wasimamao mbele yako sikuzote, wakisikia hekima yako. Na ahimidiwe Bwana, Mungu wako, aliyependezwa nawe, ili akuweke juu ya kiti chake cha enzi, kuwa mfalme wake Bwana, Mungu wako; kwa kuwa Mungu wako amewapenda Israeli, kuwathibitisha milele, kwa hiyo amekufanya kuwa mfalme juu yao, ufanye hukumu na haki.”

Malkia wa Sheba atasimama na watu wa kizazi hiki.

Luka 11:31Malkia wa Kusini ataondoka siku ya hukumu pamoja na watu wa kizazi hiki, naye atawahukumu kuwa na hatia; kwa sababu yeye alikuja kutoka ncha za dunia aisikie hekima ya Sulemani; na hapa pana mkubwa kuliko Sulemani.”

Yesu alimsifia na kumtaja malikia wa Sheba ya kuwa atasimama siku ya hukumu na watu wa kizazi hiki na kuwapa hatia kwa sababu yeye alitoka mbali kwaajili ya hekima ya Suleimani ili hali sisi tunaye Yesu na mafundisho yake ambaye ni mkuu kuliko Suleimani, Sifa kubwa sana aliyo nayo malikia huyu ni moyo wake wa kuitafuta hekima bila kujali kuwa ataipatia wapi lakini alilazimika kusafiri safari ndefu sana ilhali yeye ni mwanamke lakini hakujali kama kuitafuta hekima hiyo kungemgharimu mambo mangapi.

Wako watu wanasikia ujumbe wa Yesu Kristo ambao unahubiriwa kila iitwapo leo, wanaona na kusikia mafundisho kuhusu maswala mbalimbali ya kweli za injili lakini wanapuuzia na hawajali, Malikia aliona kuwa habari za Mungu kupitia Suleimani zilikuwa ni za Muhimu kuliko mali, aliamua kuiacha inchi yake kwa Muda kwa sababu ya kujifunza, aligundua kuwa Mungu ndiye chanzo cha Hekima yote kwani alielewa kuwa hata Hekima aliyokuwa nayo Suleimani inatoka kwa Mungu alikubali kuwa Mungu anawapenda wayahudi, alimtukuza Mungu na kumuabudu.

1Wafalme 10:9Na ahimidiwe Bwana, Mungu wako, aliyependezwa nawe, ili akuweke juu ya kiti cha enzi cha Israeli; kwa kuwa Bwana amewapenda Israeli milele, kwa hiyo amekufanya kuwa mfalme, ufanye hukumu na haki.”

 

Hitimisho:

Malikia wa Sheba ni miongoni mwa wanawake mashuhuri wa kibiblia, alikuwa ni mwanamke mwenye ujasiri, uthubutu, busara hekima na uaminifu, Yesu alimthibitisha kwa neno lake na kumtumia kama mfano wa kuigwa na kutuonya kwamba ni lazima tumsikilize Yesu ambaye yeye ni Mwana wa Mungu na kwa kumsikiliza Kristo tunajiokoa na hukumu ile ijayo, ni lazima tufanye kila jitihada kujifunza na kuitafuta kweli kama alivyofanya Malikia wa Sheba, tuache uvivu wa kujifunza neno la Mungu, tuache uvivu na kutokuacha kuhudhuria ibada, tuutafute uwepo wa Mungu na kujifunza kutoka kwake kwa gharama yoyote, tumtafute Yesu, tumtafakari, tujifunze kuhusu Yesu na wakati mwingine tuingie gharama hata za kifedha kuyatafuta maarifa sahihi kuhusu Mungu na Neema ya Mungu itatufunika na uwepo wake tutauona na kumhimidi Mungu kwa upendo wake mkubwa kwetu.

 

Na. Rev. Innocent Samuel Kamote.

Mkuu wa wajenzi mwenye Hekima.