Zaburi 34:18-19 “Walilia, naye Bwana
akasikia, Akawaponya na taabu zao zote. Bwana yu karibu nao waliovunjika moyo,
Na waliopondeka roho huwaokoa. Mateso ya mwenye haki ni mengi, Lakini Bwana
humponya nayo yote.”
Utangulizi:
Wengi wetu tunapokuwa tunapita
katika nyakati ngumu za majaribu ya aina mbalimbali, huwa tunakumbwa na mawazo
ya kufikiria kuwa huenda Mungu yuko mbali sana, na wako watu wengine duniani
hufikiri kuwa haiwezekani kabisa kuwa na ukaribu na Mungu wala hatuwezi kamwe
kuwa na ushirika na yeye, na kwa bahati mbaya hata unapokosea watu wengine
hufikiri kuwa Mungu hawezi kuwa karibu na wewe na wanadhani Mungu atakuwa
amekuacha, Kila mwanadamu aliyeumbwa na Mungu,Mungu huwa karibu naye lakini
zaidi sana aaminiye na wale waliovunjika moyo! au wanaojinyenyekeza.
·
Mungu
anapoonekana kuwa mbali!
·
Mungu si
Mungu aliye mbali
·
Jinsi ya
kuwa karibu na Mungu
Mungu anapoonekana kuwa mbali!
Hisia za kuhisi kuwa Mungu yuko
mbali zinaweza kuchangiwa na sababu mbalimbali katika maisha ya mwanadamu,
wakati mwingine kwa sababu ya mapungufu ya kibinadamu tuliyonayo, Upweke, na
changamoto mbalimbali katika maisha zinapokuwa zimetusonga mioyo yetu na hisia
zetu huhisi kuachwa na kufikiri kuwa Mungu yuko mbali na wakati mwingine kwa
sababu ya kushuka kwa Imani zetu na tafasiri zetu za kimazingira, tunapolemewa
na mawazo, mashaka, hofu na kukosa usalama tunaanza kufikiri kuwa Mungu yuko
mbali nasi au ametuacha, na wakati mwingine kudhani kuwa wala hajibu maombi
yetu pale anapochelewa kutoa msaada, ndani yetu kuna kilio mbona umeniacha
Zaburi 22:1-11 “Mungu wangu, Mungu wangu,
Mbona umeniacha? Mbona U mbali na wokovu wangu, Na maneno ya kuugua kwangu? Ee
Mungu wangu, nalia mchana lakini hujibu Na wakati wa usiku lakini sipati raha.
Na Wewe U Mtakatifu, Uketiye juu ya sifa za Israeli. Baba zetu walikutumaini
Wewe, Walitumaini, na Wewe ukawaokoa. Walikulilia Wewe wakaokoka, Walikutumaini
wasiaibike. Lakini mimi ni mdudu wala si mtu, Laumu ya wanadamu na mzaha wa
watu. Wote wanionao hunicheka sana, Hunifyonya, wakitikisa vichwa vyao; Husema,
Umtegemee Bwana; na amponye; Na amwokoe sasa, maana apendezwa naye.Naam, Wewe
ndiwe uliyenitoa tumboni, Ulinitumainisha matitini mwa mama yangu. Kwako
nalitupwa tangu tumboni, Toka tumboni mwa mamangu ndiwe Mungu wangu. Usiwe
mbali nami maana taabu i karibu, Kwa maana hakuna msaidizi.”
Zaburi 10:1-2 “Ee Bwana, kwa nini wasimama
mbali? Kwani kujificha nyakati za shida? Kwa kiburi chake asiye haki mnyonge
anafuatiwa kwa ukali; Na wanaswe kwa hila zizo hizo walizoziwaza.”
Mungu huonekana kuwa mbali
tunapougua na akachelewa kuleta uponyaji, huonekana kuwa mbali tunapolia na
akachelewa kuleta msaada, anaonekana kuwa mbali tunapopatwa na aibu ambayo yeye
angeweza kuizuia, anaonekana kuwa mbali wakati adui zetu wanapofurahi na
kutucheka ilihali yeye yupo, anaonekana kuwa mbali tunaposhutumiwa kwaajili ya
uhusiano wetu na Yeye na Yeye haonyeshi nguvu zake upesi, anaonekana kuwa mbali
wakati tuna shida na haonekani kufanya kitu au anapochelewa kufanya jambo kwa
wakati wa moyo wa kibinadamu unapotamani kufanyiwa ni kawaida tu ya kibinadamu,
kiroho na kisaikolojia kufikiria kuwa Mungu amemuacha kwa sababu wakati
mwingine tunahitaji msaada wa haraka kisha yeye akaonekana kuwa amechelewa!
Yohana 11:1-6 “Basi mtu mmoja alikuwa
hawezi, Lazaro wa Bethania, mwenyeji wa mji wa Mariamu na Martha, dada yake.
Ndiye Mariamu yule aliyempaka Bwana marhamu, akamfuta miguu kwa nywele zake,
ambaye Lazaro nduguye alikuwa hawezi. Basi wale maumbu wakatuma ujumbe kwake
wakisema, Bwana, yeye umpendaye hawezi. Naye Yesu aliposikia, alisema, Ugonjwa
huu si wa mauti, bali ni kwa ajili ya utukufu wa Mungu, ili Mwana wa Mungu
atukuzwe kwa huo. Naye Yesu alimpenda Martha na umbu lake na Lazaro.Basi
aliposikia ya kwamba hawezi, alikaa bado siku mbili pale pale alipokuwapo.”
Yesu alipewa taarifa mapema
kwamba rafiki yako umpendaye hawezi yaani anaumwa sana Lakini hata hivyo Yesu
hakufanya haraka kwenda maandiko yanaonyesha aliendelea kukaa siku mbili zaidi
akiendelea na shughuli zake, hii iliwaletea fadhaa sana Martha na Mariamu,
kwani walidhani kuwa kama Yesu angewahi hali isingelikuwa mbaya kiasi kile
lakini Yesu alionekana kuchelewa, huwa unajisikiaje Mungu anapokawia kujibu
maombi yako, unajisikiaje anapokawia kushughulika na yale yanayokusibu, au pale
anapoonekana kana kwamba hashughulikii lolote huonekana kana kwamba alikuwa
mbali hapo moyo wa mwanadamu husikitika na kuona kama kwamba Mungu yuko mbali!
Yohana 11:20-26 “Basi Martha aliposikia
kwamba Yesu anakuja, alikwenda kumlaki; na Mariamu alikuwa akikaa nyumbani.
Basi Martha akamwambia Yesu, Bwana, kama ungalikuwapo hapa, ndugu yangu
hangalikufa. Lakini hata sasa najua ya kuwa yo yote utakayomwomba Mungu, Mungu
atakupa. Yesu akamwambia, Ndugu yako atafufuka. Martha akamwambia, Najua ya
kuwa atafufuka katika ufufuo siku ya mwisho. Yesu akamwambia, Mimi ndimi huo
ufufuo, na uzima. Yeye aniaminiye mimi, ajapokufa, atakuwa anaishi; naye kila
aishiye na kuniamini hatakufa kabisa hata milele. Je! Unayasadiki hayo?”
Mungu alionekana kuwa mbali na
familia ya Matha na Mariamu hata pamoja na kuwa ilikuwa ni familia ambayo Yesu
alikuwa anawapenda sana, na ni ukweli ulio wazi kuwa kulikuwa na sauti ya
lawama kutoka kwa Martha kuwa kama ungelikuwepo hapa ndugu yangu hangalikufa,
yaani Yesu hakuwa karibu na kwa sababu alikuwa mbali amechelewa kujihusisha na
taabu ya familia hii, huu ndio mtazamo wetu, wengi wetu pale Mungu anapoonekana
kuchelewa kutoa mrejesho wa kile tunachokitarajia kutoka kwake, Mungu huonekana
kuwa mbali. Lakini Mungu si Mungu aliye mbali!
Mungu si Mungu aliye mbali.
Neno la Mungu linazungumza kinyume
na hisia zetu, lenyewe tofauti na mawazo yetu linakanusha kuwa yeye hayuko
mbali na Mungu anajitambulisha katika neno lake kuwa ni Mungu aliye karibu:-
Yeremia 23:23-24 “Mimi ni Mungu aliye
karibu, asema Bwana, mimi si Mungu aliye mbali. Je, mtu ye yote aweza kujificha
mahali pa siri, nisimwone? Asema Bwana. Je! Mbingu na nchi hazikujawa nami?
Asema Bwana.”
Mungu anaweza kufikiwa na mtu
yeyote na wakati wowote anaweza kuona hata yale tunayoyawaza kwa siri na kufikiri
mioyoni mwetu yeye ni Mungu ambaye yuko mahali kote kwa wakati mmoja na anaweza kuonekana na kupatikana kwa yeyote
yule na anasikia, tunajua tu kuwa hatuwezi kumpangia kile tunachotaka hatuwezi
kuingilia mapenzi yake lakini tunaweza kuliitia jina lake na akasikia na
kujidhihirisha katika maisha yetu.
Zaburi 145:17-19 “Bwana ni mwenye haki
katika njia zake zote, Na mwenye fadhili juu ya kazi zake zote. Bwana yu karibu
na wote wamwitao, Wote wamwitao kwa uaminifu. Atawafanyia wamchao matakwa yao,
Naye atakisikia kilio chao na kuwaokoa.”
Mungu ameahidi katika neno lake
katika torati ya kuwa hatatuacha atakuwa pamoja nasi na hatatuacha kamwe kwa
sababu hiyo hatupaswi kuogopa lolote wala hatupaswi kuacha kumuamini
Kumbukumbu 31:6 “Iweni hodari na moyo wa
ushujaa, msiogope wala msiwahofu; kwa maana Bwana, Mungu wako, yeye ndiye
anayekwenda pamoja nawe, hatakupungukia wala kukuacha.”
Mungu amehahidi katika neno lake
kutoka kwa manabii ya kuwa tusigope yeye ni Mungu wetu na kuwa atatutia nguvu
na kutusaidia na kutushika kwa mkono wake wa kuume, hivyo tusifadhaike katu
Isaya 41:10-13 “usiogope, kwa maana mimi ni
pamoja nawe; usifadhaike, kwa maana mimi ni Mungu wako; nitakutia nguvu, naam,
nitakusaidia, naam, nitakushika kwa mkono wa kuume wa haki yangu. Tazama, wote
walioona hasira juu yako watatahayarika na kufadhaika; watu washindanao nawe
watakuwa si kitu, na kuangamia. Utawatafuta wala hutawaona wale wapiganao nawe;
watakuwa si kitu; watakuwa kama kitu kisichokuwa, wale waliofanya vita juu
yako. Kwa maana mimi, Bwana, Mungu wako, nitakushika mkono wako wa kuume,
nikikuambia, Usiogope; mimi nitakusaidia.”
Mungu wakati wote anatamani
kuingilia kati mfumo wa maisha yetu pale tunaposumbuliwa na yuko tayari kutoa
msaada, faraja nguvu, muongozo, uponyaji na hata kuingilia kati kama kuna vita
na kukulipia kisasi unachopaswa wewe ni kumkaribia yeye na kuwa na agano naye
kupitia mwanaye Yesu Kristo!
Yakobo 4:7-10 “Basi mtiini Mungu. Mpingeni
Shetani, naye atawakimbia. Mkaribieni Mungu, naye atawakaribia ninyi. Itakaseni
mikono yenu, enyi wenye dhambi, na kuisafisha mioyo yenu, enyi wenye nia mbili.
Huzunikeni na kuomboleza na kulia. Kucheka kwenu na kugeuzwe kuwa kuomboleza,
na furaha yenu kuwa hamu. Jidhilini mbele za Bwana, naye atawakuza.”
Jinsi ya kuwa karibu na Mungu
Neno la Mungu sio tu
linatujulisha na kutuhimiza kuwa Mungu ni Mungu aliye karibu lakini vile vile
linatufundisha namna ya kumkaribia Bwana Mungu wetu kwa sababu hiyo pale tunapjisikia
na kudhani kuwa Mungu ametuacha yako mambo ya kufanya ili tuweze kumkaribia
naye yuko tayari kwaajili yetu!
-
Tubia
maovu na kuachana na dhambi – Isaya 59:1-2 “Tazama,
mkono wa Bwana haukupunguka, hata usiweze kuokoa wala sikio lake si zito, hata
lisiweze kusikia; lakini maovu yenu yamewafarikisha ninyi na Mungu wenu, na
dhambi zenu zimeuficha uso wake msiuone, hata hataki kusikia.”
-
Mwamini
Yesu aliye kuhani mkuu – Kazi ya kuhani mkuu ni kuomba kwaajili ya makosa
ya watu wake kwa sababu hiyo kabla hata hujaanza kufanya lolote Yesu hutuombea
kwa baba na kwa sababu hiyo tunayo haki kwa damu yake kumwendea baba kwa
ujasiri
Waebrania
10:19-23 “Basi, ndugu, kwa kuwa tuna ujasiri wa
kupaingia patakatifu kwa damu ya Yesu, njia ile aliyotuanzia iliyo mpya, iliyo
hai, ipitayo katika pazia, yaani, mwili wake; na kuwa na kuhani mkuu juu ya
nyumba ya Mungu; na tukaribie wenye moyo wa kweli, kwa utimilifu wa imani, hali
tumenyunyiziwa mioyo tuache dhamiri mbaya, tumeoshwa miili kwa maji safi. Na
mlishike sana ungamo la tumaini letu, lisigeuke; maana yeye aliyeahidi ni
mwaminifu;”
1Yohana 2:1-2 “Watoto wangu wadogo, nawaandikia haya ili kwamba msitende
dhambi. Na kama mtu akitenda dhambi tunaye Mwombezi kwa Baba, Yesu Kristo
mwenye haki, naye ndiye kipatanisho kwa dhambi zetu; wala si kwa dhambi zetu
tu, bali na kwa dhambi za ulimwengu wote.”
-
Mungu
anataka tumrudie yeye – Ni maagizo ya neno la Mungu na wito wa Mungu
mwenyewe kwamba tumrudie yeye, na tunapofanya hivyo yeye naye anaturudia sisi,
hii ni sawa tu na kusema Mungunanataka tumkaribie Yeye na Yeye atatukaribia
sisi na ameonyesha ni kwa namna gani tunaweza kumkaribia au kumrudia
Zekaria 1:3-4 “Basi, uwaambie, Bwana wa majeshi asema hivi, Nirudieni
mimi, asema Bwana wa majeshi, nami nitawarudia ninyi, asema Bwana wa majeshi.
Msiwe ninyi kama baba zenu, ambao manabii wa zamani waliwalilia, wakisema,
Bwana wa majeshi asema hivi, Rudini sasa, na kuziacha njia zenu mbovu, na
matendo yenu maovu; lakini hawakusikia, wala kunisikiliza, asema Bwana.”
Yoel 2:12-14 “Lakini hata sasa, asema Bwana, nirudieni mimi kwa mioyo
yenu yote, na kwa kufunga, na kwa kulia, na kwa kuombolea; rarueni mioyo yenu,
wala si mavazi yenu, mkamrudie Bwana, Mungu wenu; kwa maana yeye ndiye mwenye
neema, amejaa huruma; si mwepesi wa hasira, ni mwingi wa rehema, naye hughairi
mabaya. N'nani ajuaye kwamba hatarudi na kugeuka, na kutuachia baraka nyuma
yake, naam, sadaka ya unga, na sadaka ya kinywaji, kwa Bwana, Mungu wenu?”
Kama ulikuwa na hisia ya kuwa
Mungu yuko mbali, Neno la Mungu linakukumbusha kuwa Mungu ni Mungu aliye karibu
na hayuko mbali na ni Mungu ambaye anajishughulisha sana na mambo yetu, sio tu
kuwa Mungu yuko Karibu lakini kwa wale waliomwamini Yesu na kumkubali kuwa
Bwana na mwokozi katika maisha yao wafahamu kuwa anaishi ndani yetu na neno la
Mungu linasema kuwa ametupa uwezo wa kufanyika wana wa Mungu kwa sababu hiyo kama
yeye alivyo ndivyo na sisi tulivyo hapa ulimwenguni
1Yohana 3:1-3 “Tazameni, ni pendo la namna
gani alilotupa Baba, kwamba tuitwe wana wa Mungu; na ndivyo tulivyo. Kwa sababu
hii ulimwengu haututambui, kwa kuwa haukumtambua yeye. Wapenzi, sasa tu wana wa
Mungu, wala haijadhihirika bado tutakavyokuwa; lakini twajua ya kuwa
atakapodhihirishwa, tutafanana naye; kwa maana tutamwona kama alivyo. Na kila
mwenye matumaini haya katika yeye hujitakasa, kama yeye alivyo mtakatifu.”
Na Rev. Innocent Samuel Kamote
Mkuu wa wajenzi mwenye Hekima