Jumatatu, 4 Agosti 2025

Mungu anapoonekana kuwa mbali!


Zaburi 34:18-19 “Walilia, naye Bwana akasikia, Akawaponya na taabu zao zote. Bwana yu karibu nao waliovunjika moyo, Na waliopondeka roho huwaokoa. Mateso ya mwenye haki ni mengi, Lakini Bwana humponya nayo yote.”




Utangulizi:

Wengi wetu tunapokuwa tunapita katika nyakati ngumu za majaribu ya aina mbalimbali, huwa tunakumbwa na mawazo ya kufikiria kuwa huenda Mungu yuko mbali sana, na wako watu wengine duniani hufikiri kuwa haiwezekani kabisa kuwa na ukaribu na Mungu wala hatuwezi kamwe kuwa na ushirika na yeye, na kwa bahati mbaya hata unapokosea watu wengine hufikiri kuwa Mungu hawezi kuwa karibu na wewe na wanadhani Mungu atakuwa amekuacha, Kila mwanadamu aliyeumbwa na Mungu,Mungu huwa karibu naye lakini zaidi sana aaminiye na wale waliovunjika moyo! au wanaojinyenyekeza.


·         Mungu anapoonekana kuwa mbali!

·         Mungu si Mungu aliye mbali

·         Jinsi ya kuwa karibu na Mungu


Mungu anapoonekana kuwa mbali!

Hisia za kuhisi kuwa Mungu yuko mbali zinaweza kuchangiwa na sababu mbalimbali katika maisha ya mwanadamu, wakati mwingine kwa sababu ya mapungufu ya kibinadamu tuliyonayo, Upweke, na changamoto mbalimbali katika maisha zinapokuwa zimetusonga mioyo yetu na hisia zetu huhisi kuachwa na kufikiri kuwa Mungu yuko mbali na wakati mwingine kwa sababu ya kushuka kwa Imani zetu na tafasiri zetu za kimazingira, tunapolemewa na mawazo, mashaka, hofu na kukosa usalama tunaanza kufikiri kuwa Mungu yuko mbali nasi au ametuacha, na wakati mwingine kudhani kuwa wala hajibu maombi yetu pale anapochelewa kutoa msaada, ndani yetu kuna kilio mbona umeniacha

Zaburi 22:1-11 “Mungu wangu, Mungu wangu, Mbona umeniacha? Mbona U mbali na wokovu wangu, Na maneno ya kuugua kwangu? Ee Mungu wangu, nalia mchana lakini hujibu Na wakati wa usiku lakini sipati raha. Na Wewe U Mtakatifu, Uketiye juu ya sifa za Israeli. Baba zetu walikutumaini Wewe, Walitumaini, na Wewe ukawaokoa. Walikulilia Wewe wakaokoka, Walikutumaini wasiaibike. Lakini mimi ni mdudu wala si mtu, Laumu ya wanadamu na mzaha wa watu. Wote wanionao hunicheka sana, Hunifyonya, wakitikisa vichwa vyao; Husema, Umtegemee Bwana; na amponye; Na amwokoe sasa, maana apendezwa naye.Naam, Wewe ndiwe uliyenitoa tumboni, Ulinitumainisha matitini mwa mama yangu. Kwako nalitupwa tangu tumboni, Toka tumboni mwa mamangu ndiwe Mungu wangu. Usiwe mbali nami maana taabu i karibu, Kwa maana hakuna msaidizi.”

Zaburi 10:1-2 “Ee Bwana, kwa nini wasimama mbali? Kwani kujificha nyakati za shida? Kwa kiburi chake asiye haki mnyonge anafuatiwa kwa ukali; Na wanaswe kwa hila zizo hizo walizoziwaza.”

Mungu huonekana kuwa mbali tunapougua na akachelewa kuleta uponyaji, huonekana kuwa mbali tunapolia na akachelewa kuleta msaada, anaonekana kuwa mbali tunapopatwa na aibu ambayo yeye angeweza kuizuia, anaonekana kuwa mbali wakati adui zetu wanapofurahi na kutucheka ilihali yeye yupo, anaonekana kuwa mbali tunaposhutumiwa kwaajili ya uhusiano wetu na Yeye na Yeye haonyeshi nguvu zake upesi, anaonekana kuwa mbali wakati tuna shida na haonekani kufanya kitu au anapochelewa kufanya jambo kwa wakati wa moyo wa kibinadamu unapotamani kufanyiwa ni kawaida tu ya kibinadamu, kiroho na kisaikolojia kufikiria kuwa Mungu amemuacha kwa sababu wakati mwingine tunahitaji msaada wa haraka kisha yeye akaonekana kuwa amechelewa!

Yohana 11:1-6 “Basi mtu mmoja alikuwa hawezi, Lazaro wa Bethania, mwenyeji wa mji wa Mariamu na Martha, dada yake. Ndiye Mariamu yule aliyempaka Bwana marhamu, akamfuta miguu kwa nywele zake, ambaye Lazaro nduguye alikuwa hawezi. Basi wale maumbu wakatuma ujumbe kwake wakisema, Bwana, yeye umpendaye hawezi. Naye Yesu aliposikia, alisema, Ugonjwa huu si wa mauti, bali ni kwa ajili ya utukufu wa Mungu, ili Mwana wa Mungu atukuzwe kwa huo. Naye Yesu alimpenda Martha na umbu lake na Lazaro.Basi aliposikia ya kwamba hawezi, alikaa bado siku mbili pale pale alipokuwapo.”

Yesu alipewa taarifa mapema kwamba rafiki yako umpendaye hawezi yaani anaumwa sana Lakini hata hivyo Yesu hakufanya haraka kwenda maandiko yanaonyesha aliendelea kukaa siku mbili zaidi akiendelea na shughuli zake, hii iliwaletea fadhaa sana Martha na Mariamu, kwani walidhani kuwa kama Yesu angewahi hali isingelikuwa mbaya kiasi kile lakini Yesu alionekana kuchelewa, huwa unajisikiaje Mungu anapokawia kujibu maombi yako, unajisikiaje anapokawia kushughulika na yale yanayokusibu, au pale anapoonekana kana kwamba hashughulikii lolote huonekana kana kwamba alikuwa mbali hapo moyo wa mwanadamu husikitika na kuona kama kwamba Mungu yuko mbali!

Yohana 11:20-26 “Basi Martha aliposikia kwamba Yesu anakuja, alikwenda kumlaki; na Mariamu alikuwa akikaa nyumbani. Basi Martha akamwambia Yesu, Bwana, kama ungalikuwapo hapa, ndugu yangu hangalikufa. Lakini hata sasa najua ya kuwa yo yote utakayomwomba Mungu, Mungu atakupa. Yesu akamwambia, Ndugu yako atafufuka. Martha akamwambia, Najua ya kuwa atafufuka katika ufufuo siku ya mwisho. Yesu akamwambia, Mimi ndimi huo ufufuo, na uzima. Yeye aniaminiye mimi, ajapokufa, atakuwa anaishi; naye kila aishiye na kuniamini hatakufa kabisa hata milele. Je! Unayasadiki hayo?

Mungu alionekana kuwa mbali na familia ya Matha na Mariamu hata pamoja na kuwa ilikuwa ni familia ambayo Yesu alikuwa anawapenda sana, na ni ukweli ulio wazi kuwa kulikuwa na sauti ya lawama kutoka kwa Martha kuwa kama ungelikuwepo hapa ndugu yangu hangalikufa, yaani Yesu hakuwa karibu na kwa sababu alikuwa mbali amechelewa kujihusisha na taabu ya familia hii, huu ndio mtazamo wetu, wengi wetu pale Mungu anapoonekana kuchelewa kutoa mrejesho wa kile tunachokitarajia kutoka kwake, Mungu huonekana kuwa mbali. Lakini Mungu si Mungu aliye mbali!

Mungu si Mungu aliye mbali.

Neno la Mungu linazungumza kinyume na hisia zetu, lenyewe tofauti na mawazo yetu linakanusha kuwa yeye hayuko mbali na Mungu anajitambulisha katika neno lake kuwa ni Mungu aliye karibu:-

Yeremia 23:23-24 “Mimi ni Mungu aliye karibu, asema Bwana, mimi si Mungu aliye mbali. Je, mtu ye yote aweza kujificha mahali pa siri, nisimwone? Asema Bwana. Je! Mbingu na nchi hazikujawa nami? Asema Bwana.”          

Mungu anaweza kufikiwa na mtu yeyote na wakati wowote anaweza kuona hata yale tunayoyawaza kwa siri na kufikiri mioyoni mwetu yeye ni Mungu ambaye yuko mahali kote kwa wakati mmoja  na anaweza kuonekana na kupatikana kwa yeyote yule na anasikia, tunajua tu kuwa hatuwezi kumpangia kile tunachotaka hatuwezi kuingilia mapenzi yake lakini tunaweza kuliitia jina lake na akasikia na kujidhihirisha katika maisha yetu.

Zaburi 145:17-19 “Bwana ni mwenye haki katika njia zake zote, Na mwenye fadhili juu ya kazi zake zote. Bwana yu karibu na wote wamwitao, Wote wamwitao kwa uaminifu. Atawafanyia wamchao matakwa yao, Naye atakisikia kilio chao na kuwaokoa.”

Mungu ameahidi katika neno lake katika torati ya kuwa hatatuacha atakuwa pamoja nasi na hatatuacha kamwe kwa sababu hiyo hatupaswi kuogopa lolote wala hatupaswi kuacha kumuamini

Kumbukumbu 31:6 “Iweni hodari na moyo wa ushujaa, msiogope wala msiwahofu; kwa maana Bwana, Mungu wako, yeye ndiye anayekwenda pamoja nawe, hatakupungukia wala kukuacha.”

Mungu amehahidi katika neno lake kutoka kwa manabii ya kuwa tusigope yeye ni Mungu wetu na kuwa atatutia nguvu na kutusaidia na kutushika kwa mkono wake wa kuume, hivyo tusifadhaike katu

Isaya 41:10-13 “usiogope, kwa maana mimi ni pamoja nawe; usifadhaike, kwa maana mimi ni Mungu wako; nitakutia nguvu, naam, nitakusaidia, naam, nitakushika kwa mkono wa kuume wa haki yangu. Tazama, wote walioona hasira juu yako watatahayarika na kufadhaika; watu washindanao nawe watakuwa si kitu, na kuangamia. Utawatafuta wala hutawaona wale wapiganao nawe; watakuwa si kitu; watakuwa kama kitu kisichokuwa, wale waliofanya vita juu yako. Kwa maana mimi, Bwana, Mungu wako, nitakushika mkono wako wa kuume, nikikuambia, Usiogope; mimi nitakusaidia.”

Mungu wakati wote anatamani kuingilia kati mfumo wa maisha yetu pale tunaposumbuliwa na yuko tayari kutoa msaada, faraja nguvu, muongozo, uponyaji na hata kuingilia kati kama kuna vita na kukulipia kisasi unachopaswa wewe ni kumkaribia yeye na kuwa na agano naye kupitia mwanaye Yesu Kristo!

Yakobo 4:7-10 “Basi mtiini Mungu. Mpingeni Shetani, naye atawakimbia. Mkaribieni Mungu, naye atawakaribia ninyi. Itakaseni mikono yenu, enyi wenye dhambi, na kuisafisha mioyo yenu, enyi wenye nia mbili. Huzunikeni na kuomboleza na kulia. Kucheka kwenu na kugeuzwe kuwa kuomboleza, na furaha yenu kuwa hamu. Jidhilini mbele za Bwana, naye atawakuza.”

Jinsi ya kuwa karibu na Mungu

Neno la Mungu sio tu linatujulisha na kutuhimiza kuwa Mungu ni Mungu aliye karibu lakini vile vile linatufundisha namna ya kumkaribia Bwana Mungu wetu kwa sababu hiyo pale tunapjisikia na kudhani kuwa Mungu ametuacha yako mambo ya kufanya ili tuweze kumkaribia naye yuko tayari kwaajili yetu!

-          Tubia maovu na kuachana na dhambi – Isaya 59:1-2 “Tazama, mkono wa Bwana haukupunguka, hata usiweze kuokoa wala sikio lake si zito, hata lisiweze kusikia; lakini maovu yenu yamewafarikisha ninyi na Mungu wenu, na dhambi zenu zimeuficha uso wake msiuone, hata hataki kusikia.”

 

-          Mwamini Yesu aliye kuhani mkuu – Kazi ya kuhani mkuu ni kuomba kwaajili ya makosa ya watu wake kwa sababu hiyo kabla hata hujaanza kufanya lolote Yesu hutuombea kwa baba na kwa sababu hiyo tunayo haki kwa damu yake kumwendea baba kwa ujasiri

 

Waebrania 10:19-23 “Basi, ndugu, kwa kuwa tuna ujasiri wa kupaingia patakatifu kwa damu ya Yesu, njia ile aliyotuanzia iliyo mpya, iliyo hai, ipitayo katika pazia, yaani, mwili wake; na kuwa na kuhani mkuu juu ya nyumba ya Mungu; na tukaribie wenye moyo wa kweli, kwa utimilifu wa imani, hali tumenyunyiziwa mioyo tuache dhamiri mbaya, tumeoshwa miili kwa maji safi. Na mlishike sana ungamo la tumaini letu, lisigeuke; maana yeye aliyeahidi ni mwaminifu;”

 

1Yohana 2:1-2 “Watoto wangu wadogo, nawaandikia haya ili kwamba msitende dhambi. Na kama mtu akitenda dhambi tunaye Mwombezi kwa Baba, Yesu Kristo mwenye haki, naye ndiye kipatanisho kwa dhambi zetu; wala si kwa dhambi zetu tu, bali na kwa dhambi za ulimwengu wote.”

 

-          Mungu anataka tumrudie yeye – Ni maagizo ya neno la Mungu na wito wa Mungu mwenyewe kwamba tumrudie yeye, na tunapofanya hivyo yeye naye anaturudia sisi, hii ni sawa tu na kusema Mungunanataka tumkaribie Yeye na Yeye atatukaribia sisi na ameonyesha ni kwa namna gani tunaweza kumkaribia au kumrudia

 

Zekaria 1:3-4 “Basi, uwaambie, Bwana wa majeshi asema hivi, Nirudieni mimi, asema Bwana wa majeshi, nami nitawarudia ninyi, asema Bwana wa majeshi. Msiwe ninyi kama baba zenu, ambao manabii wa zamani waliwalilia, wakisema, Bwana wa majeshi asema hivi, Rudini sasa, na kuziacha njia zenu mbovu, na matendo yenu maovu; lakini hawakusikia, wala kunisikiliza, asema Bwana.”

 

Yoel 2:12-14 “Lakini hata sasa, asema Bwana, nirudieni mimi kwa mioyo yenu yote, na kwa kufunga, na kwa kulia, na kwa kuombolea; rarueni mioyo yenu, wala si mavazi yenu, mkamrudie Bwana, Mungu wenu; kwa maana yeye ndiye mwenye neema, amejaa huruma; si mwepesi wa hasira, ni mwingi wa rehema, naye hughairi mabaya. N'nani ajuaye kwamba hatarudi na kugeuka, na kutuachia baraka nyuma yake, naam, sadaka ya unga, na sadaka ya kinywaji, kwa Bwana, Mungu wenu?                      

 

Kama ulikuwa na hisia ya kuwa Mungu yuko mbali, Neno la Mungu linakukumbusha kuwa Mungu ni Mungu aliye karibu na hayuko mbali na ni Mungu ambaye anajishughulisha sana na mambo yetu, sio tu kuwa Mungu yuko Karibu lakini kwa wale waliomwamini Yesu na kumkubali kuwa Bwana na mwokozi katika maisha yao wafahamu kuwa anaishi ndani yetu na neno la Mungu linasema kuwa ametupa uwezo wa kufanyika wana wa Mungu kwa sababu hiyo kama yeye alivyo ndivyo na sisi tulivyo hapa ulimwenguni

1Yohana 3:1-3 “Tazameni, ni pendo la namna gani alilotupa Baba, kwamba tuitwe wana wa Mungu; na ndivyo tulivyo. Kwa sababu hii ulimwengu haututambui, kwa kuwa haukumtambua yeye. Wapenzi, sasa tu wana wa Mungu, wala haijadhihirika bado tutakavyokuwa; lakini twajua ya kuwa atakapodhihirishwa, tutafanana naye; kwa maana tutamwona kama alivyo. Na kila mwenye matumaini haya katika yeye hujitakasa, kama yeye alivyo mtakatifu.”

Na Rev. Innocent Samuel Kamote

Mkuu wa wajenzi mwenye Hekima

Jumapili, 27 Julai 2025

Mungu anaposhika Kalamu!

 

Esta 3:8-11 “Basi Hamani akamwambia mfalme Ahasuero, Kuna taifa moja waliotawanyika na kukaa mahali mahali katikati ya mataifa walioko katika majimbo yote ya ufalme wako. Nao sheria zao zimefarakana na sheria za kila taifa; wala hawazishiki amri za mfalme; kwa hiyo haimpasi mfalme kuchukuliana nao. Basi, mfalme akiona vema, na iandikwe kwamba waangamizwe; nami nitalipa talanta kumi elfu za fedha mikononi mwao watakaosimamia shughuli hiyo, waziweke katika hazina ya mfalme. Ndipo mfalme alipoivua pete yake mkononi, akampa Hamani bin Hamedatha, Mwagagi, adui ya Wayahudi. Kisha mfalme akamwambia Hamani, Hiyo fedha umepewa, na watu pia, fanya uonavyo vema.”

 


Utangulizi:

Mungu anaposhika kalamu ni usemi wa fumbo (Metaphor)  unaotumika kuelezea uwezo na utendaji wa Mungu katika kuamua mambo ya kitaifa, ulimwengu au mtu mmoja mmoja kuhusiana na mpango wake wa baadaye, Mungu ndiye mshika dau wa maisha ya kila mtu na anayeujua mwanzo na mwisho wa mtu au anayeamua kuwa hatima ya mtu itakuwaje, uweza wake huo hauwezi kuingiliwa wala kuathiriwa na mpango wowote wa kibinadamu wala Shetani, wakati wote yeye ndiye hubakia kuwa mwenye hatima ya mwisho wa kila mtu, familia, taifa na ulimwengu!, Hakuna mwanadamu, wala serikali wala ufalme wala mamlaka yenye uwezo wa kuamua hatima yako itakuwaje isipokuwa Mungu peke yake! Ni yeye peke yake ndiye anayetuwazia mema kwa sababu yeye ndiye aliye tuumba na kwa sababu hiyo anajua hatima yetu na sababu ya yeye kutuumba! Ameandika kila kitu kutuhusu hakuna wa kufuta.

Yeremia 29:11 “Maana nayajua mawazo ninayowawazia ninyi, asema Bwana, ni mawazo ya amani wala si ya mabaya, kuwapa ninyi tumaini siku zenu za mwisho.”

Kwa bahati mbaya wako watu duniani ambao hufiriki ya kuwa wao wanaweza kuamua hatima ya maisha yako au maisha yetu au kwamba hatima ya taifa letu iko mikononi mwao, na kwa sababu hiyo kwa kutumia nafasi waliyo nayo wakati mwingine wameweza kuingilia na kujaribu kuzuia au kuwakwamisha watu wengine katika mpango wa Mungu wakidhani kwa mawazo mafupi kuwa wao wanaweza kufanya hivyo, Lakini hatimaye Mungu huingilia kati na kubadilisha mambo ni mpango wake peke yake unaoweza kuhitimisha mambo kinyume na matarajio na mipango ya wanadamu ni wazo lake na shauri lake na kusudi lake pekee linaloweza kusimama.

Zaburi 33:8-11 “Nchi yote na imwogope Bwana, Wote wakaao duniani na wamche. Maana Yeye alisema, ikawa; Na Yeye aliamuru, ikasimama. Bwana huyabatilisha mashauri ya mataifa, Huyatangua makusudi ya watu. Shauri la Bwana lasimama milele, Makusudi ya moyo wake vizazi na vizazi.”

Leo basi tutachukua muda mfupi, kujifunza kwa kina na mapana ujumbe huu wa muhimu “Mungu anaposhika kalamu”na tutajifunza ujumbe huu kwa kuzingatia vipengele viwili muhimu vifuatavyo:-

·         Njama za kuharibiwa kwa hatima yako.

·         Mungu anaposhika kalamu.


Njama za kuharibiwa kwa hatima yako

Katika dunia hii iliyojaa iliyojawa na watu wenye chuki, uadui, uchawi, wivu, hasira, faraka uzushi, husuda, ulafi, tamaa mbaya, chuki zisizo hata na sababu majungu na fitina, kuharibiana na kuchafuana, kuwindana na kutafutana watu wanaweza kwa sababu au hata bila sababu kukutafutia namna ya kukutengenezea hatima mbaya, adui zako watatamani wakati wote wasikie unaharibikiwa na mambo yako hayaendi na wakati mwingine watakusudia uwe na hatima mbaya hata kinyume na mapenzi ya Mungu, watatamani kuona ndoto zako, maono yako na matamanio yako uliyopewa na Mungu hayatimii kwa mbinu na hila za kibinadamu, kwa hiyo unaweza kuwekewa mpango mkakati na watu ili wahakikishe ya kuwa mambo yako yanakwama, kama haya yanakukuta hilo sio jambo geni kwako wala kwetu, maandiko yanatutia moyo kuwa tusione kuwa ni ajabu tunapopatwa na changamoto za aina mbalimbali

1Petro 4:12-13 “Wapenzi, msione kuwa ni ajabu ule msiba ulio kati yenu, unaowapata kama moto ili kuwajaribu, kana kwamba ni kitu kigeni kiwapatacho. Lakini kama mnavyoyashiriki mateso ya Kristo, furahini; ili na katika ufunuo wa utukufu wake mfurahi kwa shangwe.”

Nyakati za Biblia walikuweko watu kama wewe na wanadamu kama wewe waliokutana na changamoto kama zako watu wakiwakusudia kuwakwamisha kwaajili ya maslahi yao au kwa sababu ya husuda ya kitu cha kiungu ambacho Mungu amekiweka ndani yako:-

1.       Yusufu – Mungu alimpa ndoto kubwa za maisha yake ya baadae,  na ya nduguze lakini sio hivyo tu alipata kibali kwa Mungu na kwa baba yake, Mungu alimpenda Yusufu na alikuwa pamoja naye, lakini pia baba yake alimpenda sana na Mungu alimpa Yusufu ndoto kuhusu hatima yake lakini hata hivyo nduguze walichukizwa na ndoto hizo na kuanza kula njama ya kutaka kumuangamiza.

 

Mwanzo 37:2-11 “Hivi ndivyo vizazi vya Yakobo. Yusufu, aliyekuwa mwenye miaka kumi na saba, alikuwa akichunga kondoo pamoja na ndugu zake; naye alikuwa kijana pamoja na wana wa Bilha, na wana wa Zilpa, wake wa baba yake. Yusufu akamletea baba yao habari zao mbaya. Basi Israeli akampenda Yusufu kuliko wanawe wote, maana ni mwana wa uzee wake, akamfanyia kanzu ndefu. Ndugu zake wakaona ya kuwa baba yao anampenda kuliko ndugu zake wote, wakamchukia, wala hawakuweza kusema naye kwa amani. Yusufu akaota ndoto, akawapa ndugu zake habari, nao wakazidi kumchukia; akawaambia, Tafadhalini, sikieni ndoto hii niliyoiota. Tazama, sisi tulikuwa tukifunga miganda shambani, kumbe! Mganda wangu ukaondoka ukasimama, na tazama, miganda yenu ikazunguka ikainama mbele ya mganda wangu. Ndugu zake wakamwambia, Je! Kweli wewe utatumiliki sisi? Nawe utatutawala sisi? Wakazidi kumchukia kwa ajili ya ndoto yake, na kwa maneno yake. Akaota tena ndoto nyingine, akawaambia ndugu zake, akasema, Angalieni, nimeota ndoto nyingine; na tazama, jua na mwezi na nyota kumi na moja zikaniinamia. Akawaambia baba yake na ndugu zake; baba yake akamkemea akamwambia, Ni ndoto gani hii uliyoiota? Je! Mimi na mama yako na ndugu zako tutakuja tukusujudie hata nchi? Ndugu zake wakamhusudu; bali baba yake akalihifadhi neno hili.”

 

Ni jambo la kushangaza kwamba Yusufu alichukiwa na ndugu zake na sio kumchukia tu walimuhusudu walikuwa na wivu wenye uchungu mkubwa dhidi yake na kwa sababu ya ndoto zake walihakikisha wanaweka mkakati wa kummaliza ili waone ndoto zake zitatimiaje yaani walitaka kumuua!

 

Mwanzo 37:13-20 “Israeli akamwambia Yusufu, Je! Ndugu zako hawachungi kondoo katika Shekemu? Njoo, nikutume kwao. Akamwambia, Mimi hapa. Akamwambia, Enenda, basi, ukaone kama ndugu zako hawajambo, na kundi nalo li salama, ukaniletee habari. Basi akampeleka kutoka bonde la Hebroni, akafika Shekemu. Mtu mmoja akamkuta, naye alikuwa anazunguka-zunguka katika nyika; yule mtu akamwuliza, akisema, Unatafuta nini? Akasema, Nawatafuta ndugu zangu; tafadhali uniambie mahali wanakochunga. Yule mtu akasema, Wametoka hapa, maana niliwasikia wakisema, Twendeni Dothani. Basi Yusufu akawafuata ndugu zake akawakuta huko Dothani. Wakamwona toka mbali, na kabla hajawakaribia, wakafanya shauri juu yake ili wamwue. Wakasemezana wao kwa wao, Tazama, yule bwana wa ndoto anakuja. Haya, twende, tukamwue na kumtupa katika birika mojawapo, nasi tutasema, Mnyama mkali amemla; kisha tutaona zitakuwaje ndoto zake.”

 

Wanadamu bila kufahamu kuwa Mungu alikwisha kumuandikia mtumishi wake Yusufu kuwa atakuwa mkuu, wao walikuwa wakijaribu kuandika kinyume na kile ambacho Mungu alikuwa amekikusudia kwa Yusufu, ndugu yangu hayo unayoyapitia ni kuwa wanadamu wanataka kujaribu kuandika hitoria yako kinyume na kile ambacho Mungu amekikusudia katika maisha yako!

 

2.       Daniel – Alifanyiwa njama na Mawaziri wenzake  baada ya kuwa ameinuliwa sana na Mungu na kupata kibali kwa mfalme ambaye aliamua kumuweka juu sana katika madaraka ya nchi ya uhamishoni, Mawaziri wa kikaldayo walikuwa na mpango wa kuharibu hatima ya Daniel na kwa kuwa alikuwa na uadilifu walikosa sababu, wakaona watumie njama ya kuzuia maombi kwa Mungu aliye hai, jambo ambalo lingesababisha Daniel ashindwe na kupata sababu ya kumhukumu kwa hiyo mawaziri waliandika mswada na kuupitisha

 

Daniel 6:1-16 “Ilimpendeza Dario kuweka juu ya ufalme maliwali mia na ishirini, wawe juu ya ufalme wote; na juu yao akaweka wakubwa watatu, na Danieli alikuwa mmoja wao; ili maliwali hawa watoe hesabu kwao, mfalme asipate hasara. Basi Danieli huyo alipata sifa kuliko wakubwa na maliwali, kwa kuwa roho bora ilikuwa ndani yake; naye mfalme akaazimu kumweka juu ya ufalme wote. Basi mawaziri na maamiri wakatafuta sana kupata sababu za kumshitaki Danieli kwa habari za mambo ya ufalme; lakini hawakuweza kuona sababu wala kosa; kwa maana alikuwa mwaminifu, wala halikuonekana kosa wala hatia ndani yake. Ndipo wale watu wakasema, Hatutapata sababu ya kumshitaki Danieli huyo, tusipoipata katika mambo ya sheria ya Mungu wake. Basi wale mawaziri na maamiri wakakusanyika pamoja mbele ya mfalme, wakamwambia hivi, Mfalme Dario, uishi milele. Mawaziri wote wa ufalme, na manaibu, na maamiri, na madiwani, na maliwali wamefanya shauri pamoja ili kuweka amri ya kifalme; na kupiga marufuku, ya kwamba mtu ye yote atakayeomba dua kwa Mungu awaye yote, au kwa mtu awaye yote, katika muda wa siku thelathini, ila kwako, Ee mfalme atatupwa katika tundu la simba. Sasa, Ee mfalme, piga marufuku, ukatie sahihi maandiko haya, yasibadilike, kama ilivyo sheria ya Wamedi na Waajemi, isiyoweza kubadilika. Basi mfalme Dario akayatia sahihi maandiko yale, na ile marufuku. Hata Danieli, alipojua ya kuwa yale maandiko yamekwisha kutiwa sahihi, akaingia nyumbani mwake, (na madirisha katika chumba chake yalikuwa yamefunguliwa kukabili Yerusalemu;) akapiga magoti mara tatu kila siku, akasali, akashukuru mbele za Mungu wake, kama alivyokuwa akifanya tokea hapo. Basi watu hao wakakusanyika pamoja, wakamwona Danieli akiomba dua, na kusihi mbele za Mungu wake. Ndipo wakakaribia, wakasema mbele ya mfalme katika habari ya ile marufuku ya mfalme; Je! Hukuitia sahihi ile marufuku, ya kwamba kila mtu atakayeomba dua kwa Mungu awaye yote, au kwa mtu awaye yote, katika muda wa siku thelathini, ila kwako, Ee mfalme, atatupwa katika tundu la simba? Mfalme akajibu, akasema, Neno hili ni kweli, kama ilivyo sheria ya Wamedi na Waajemi isiyoweza kubadilika. Basi wakajibu, wakasema mbele ya mfalme, Yule Danieli, aliye mmoja wa wana wa wale waliohamishwa wa Yuda, hakujali wewe, Ee mfalme, wala ile marufuku uliyoitia sahihi, bali aomba dua mara tatu kila siku. Basi mfalme aliposikia maneno haya alikasirika sana, akakaza moyo wake ili kumponya Danieli; akajitaabisha kumwokoa hata jua likachwa. Ndipo watu wale wakakusanyika pamoja mbele ya mfalme, wakamwambia mfalme, Ee mfalme, ujue ya kuwa ni sheria ya Wamedi na Waajemi, lisibadilike neno lo lote lililo marufuku, wala amri yo yote iliyowekwa na mfalme. Basi mfalme akatoa amri, nao wakamleta Danieli, wakamtupa katika tundu la simba. Mfalme akanena, akamwambia Danieli, Mungu wako unayemtumikia daima, yeye atakuponya.”

 

3.       Wayahudi waliokuwa uhamishoni – Mungu alikuwa amewabarikia sana wayahudi waliokuwa utumwani, wao walikuwa na moyo ule ule wa kumcha Mungu wakiwa wamejifunza kwamba kupitia kuabudu miungu mingine wao walihukumiwa kwenda utumwani kwa hiyo wayahudi waliokuwa uhamishoni hawakutaka kuabudu sanamu wala mtu waliipeleka heshima yote kwa Mungu, Kwa sababu hiyo Hamani ambaye alikuwa amemchukia Modrekai kwa sababu alikuwa hainami mbele zake aliamua kupitisha mswada bungeni ili kwamba ipitishwe sheria ya kuwaangamiza wayahudi wote na hivyo waliandika mswada wa maangamizi

 

Esta 3:8-11 “Basi Hamani akamwambia mfalme Ahasuero, Kuna taifa moja waliotawanyika na kukaa mahali mahali katikati ya mataifa walioko katika majimbo yote ya ufalme wako. Nao sheria zao zimefarakana na sheria za kila taifa; wala hawazishiki amri za mfalme; kwa hiyo haimpasi mfalme kuchukuliana nao. Basi, mfalme akiona vema, na iandikwe kwamba waangamizwe; nami nitalipa talanta kumi elfu za fedha mikononi mwao watakaosimamia shughuli hiyo, waziweke katika hazina ya mfalme. Ndipo mfalme alipoivua pete yake mkononi, akampa Hamani bin Hamedatha, Mwagagi, adui ya Wayahudi. Kisha mfalme akamwambia Hamani, Hiyo fedha umepewa, na watu pia, fanya uonavyo vema.”

 

Hata hivyo katika namna isiyoweze kuelezeka sheraia za waamedi na waajemi zilikuwa zikipitishwa haikuwa kitu rahisi kubatilisha isipokuwa tu kama Mungu ataingilia kati kwani sharia zao zikipita zimepita

 

Esta 8:8 “Basi waandikieni Wayahudi pia vyo vyote mpendavyo, kwa jina la mfalme, mkatie muhuri kwa pete ya mfalme; kwa kuwa andiko lililoandikwa kwa jina la mfalme na kutiwa muhuri kwa pete ya mfalme hakuna awezaye kulitangua.”

 

4.       Yesu Kristo – Ambaye alishitakiwa kwa husuda na wakuu wa makuhani ili tu kumsambaratisha na wakidhani kwa kufanya hizo njama watakuwa wamemmaliza kabisa, aliandikiwa hati ya hukumu ya kufa msalabani

 

Mathayo 27:17-20 “Basi walipokutanika, Pilato akawaambia, Mnataka niwafungulie yupi? Yule Baraba, au Yesu aitwaye Kristo? Kwa maana alijua ya kuwa wamemtoa kwa husuda. Na alipokuwa ameketi juu ya kiti cha hukumu, mkewe alimpelekea mjumbe, kumwambia, Usiwe na neno na yule mwenye haki; kwa sababu nimeteswa mengi leo katika ndoto kwa ajili yake. Nao wakuu wa makuhani na wazee wakawashawishi makutano ili wamtake Baraba, na kumwangamiza Yesu.”

 

Wakati mwingine adui zako watafanya njama na kukushambulia kwa hila na njia mbalimbali ilimradi tu wahakikishe kuwa wanakupoteza au wanaharibu hatima yako kama tunavyoona katika mifano hiyo hapo juu katika maandiko, ndugu msomaji wangu na msikilizaji wangu inawezekana kuwa mara kadhaa na wewe unaweza kuwa umekutana na changamoto za aina mbalimbali ambazo zote zinalenga kumaliza au kuharibu hatima yako au hata kukuua kwa makusudi yale yale ya kuua kitu cha kiungu ambacho kimewekwa ndani yako! Lakini hata hivyo uzoefu wa kimaandiko unaonyesha ya kuwa Mungu huingilia kati na kubadilisha mambo pale anaposhika kalamu yake. Mungu huwaacha wanadamu waandike miswada yao kisha yeye kama mfalme wa wafalme huitangua, Mungu anaposhika kalamu historia yote na matarajio yote ya adui hubatilika

Mungu anaposhika kalamu.

Mungu anaposhika kalamu maana yake Mungu anauwezo wa kubadili historia ya mambo, wanadamu na shetani wanapokusudia kuharibu na kusitisha kile kitu ambacho Mungu amekiweka ndani yako au kuharibu hatima yako na kukupakazia ubaya au kukukusudia ubaya Mungu anauwezo wa kubadili historia ya mambo mabaya na kuigeuza kujwa njema, au uwezo wa kubadili maji machungu kuwa matamu, anauwezo wa kuandika upya hatima yako ya familia yako na taifa lako na hata ulimwengu kwa ujumla, Mungu anauwezo wa kurejesha heshima ambayo imeharibiwa, ana uwezo wa kuharibu mipango mibaya ya adui na kuifanya kuwa myema au kupitia mpango huo mbaya akatokeza jambo jema kwa uwezo wake mkuu na kwa mkono wake wa nguvu ulionyooshwa

Warumi 8:28-30 “Nasi twajua ya kuwa katika mambo yote Mungu hufanya kazi pamoja na wale wampendao katika kuwapatia mema, yaani, wale walioitwa kwa kusudi lake. Maana wale aliowajua tangu asili, aliwachagua tangu asili wafananishwe na mfano wa Mwana wake, ili yeye awe mzaliwa wa kwanza miongoni mwa ndugu wengi. Na wale aliowachagua tangu asili, hao akawaita; na wale aliowaita, hao akawahesabia haki; na wale aliowahesabia haki, hao akawatukuza.”

Yusufu aliyefanyiwa njama na kaka zake ili kwamba ndoto zake zisitimie Mungu aliitumia njia iiliyoonekana kuwa ya uchungu na ya kuumiza kuleta wokovu kwa taifa zima, Mungu alibadili hatima mbaya iliyokusudiwa na wanadamu kutimiza hatima yeke iliyokusudiwa na yeye Mungu anaposhika kalamu mambo hubadilika.  

Mwanzo 50:15-20 “Ndugu zake Yusufu walipoona ya kwamba baba yao amekufa, walisema, Labda Yusufu atatuchukia; naye atatulipa maovu yetu tuliyomtenda.  Wakapeleka watu kwa Yusufu, kunena, Baba yako alitoa amri kabla ya kufa kwake, akasema, Mwambieni Yusufu hivi, Naomba uwaachilie ndugu zako kosa lao na dhambi yao, maana walikutenda mabaya; sasa twakuomba utuachilie kosa la watumwa wa Mungu wa baba yako. Yusufu akalia waliposema naye. Nduguze wakaenda tena, wakamwangukia miguu, wakasema, Tazama, sisi tu watumwa wako. Yusufu akawaambia, Msiogope, je! Mimi ni badala ya Mungu? Nanyi kweli mlinikusudia mabaya, bali Mungu aliyakusudia kuwa mema, ili itokee kuokoa taifa kubwa, kama ilivyo leo.”

Mungu aliingilia kati maswala ya Daniel ambaye alishitakiwa kwa hila na Mungu aliona wazi kuwa hakuwa na hatia na mfalme akabadili mawazo kwa kumtoa Daniel katika tundu la simba na kuwaingiza washitaki wake na familia zao Ni kitu gani kilitokea Mungu alposhika kalamu makanwa ya simba hayakumuweza Daniel na badala yake adui zake walishughulikiwa!

Daniel 6:21-27. “Ndipo Danieli akamwambia mfalme, Ee mfalme, uishi milele. Mungu wangu amemtuma malaika wake, naye ameyafumba makanwa ya simba, nao hawakunidhuru; kwa kuwa mbele zake mimi nalionekana kuwa sina hatia; tena, mbele yako, Ee mfalme, sikukosa neno. Basi mfalme akafurahi sana, akaamuru wamtoe Danieli katika lile tundu. Ndipo Danieli akatolewa katika lile tundu, wala dhara lo lote halikuonekana mwilini mwake, kwa sababu alikuwa anamtumaini Mungu wake. Mfalme akaamuru, nao wakawaleta wale watu waliomshitaki Danieli, wakawatupa katika tundu la simba, wao, na watoto wao, na wake zao; na wale simba wakawashinda wakaivunja mifupa yao vipande vipande, kabla hawajafika chini ya tundu. Ndipo mfalme Dario akawaandikia watu wa kabila zote, na taifa zote, na lugha zote, waliokaa juu ya uso wa dunia; Amani na iongezeke kwenu. Mimi naweka amri, ya kwamba katika mamlaka yote ya ufalme wangu watu watetemeke na kuogopa mbele za Mungu wa Danieli; maana yeye ndiye Mungu aliye hai, adumuye milele, na ufalme wake ni ufalme usioharibika, na mamlaka yake itadumu hata mwisho. Yeye huponya na kuokoa, hutenda ishara na maajabu mbinguni na duniani, ndiye aliyemponya Danieli na nguvu za simba.”

Mungu alishika kalamu na kuondoa mashitaka dhidi ya wayahudi waliokuwa uhamishoni na wakapewa mamlaka ya kujilinda na kuwafanyia lolote adui zao, ingawa tunaona kuwa Hamani alikuwa na mpango mbaya lakini Mungu alibadili mpango huo na hata msalaba ambao Hamani alikuwa amemuandalia Mordekai ukweli ni kuwa alisulubiwa yeye

Esta 8:7-11 “Mfalme Ahasuero akawaambia malkia Esta na Mordekai, Myahudi, kusema, Tazama, nimekwisha kumpa Esta nyumba yake Hamani, naye mwenyewe wamekwisha kumtundika juu ya mti, kwa sababu aliwatia mikono Wayahudi. Basi waandikieni Wayahudi pia vyo vyote mpendavyo, kwa jina la mfalme, mkatie muhuri kwa pete ya mfalme; kwa kuwa andiko lililoandikwa kwa jina la mfalme na kutiwa muhuri kwa pete ya mfalme hakuna awezaye kulitangua. Basi, waandishi wa mfalme wakaitwa pale pale, siku ya ishirini na tatu ya mwezi wa tatu, ndio mwezi wa Siwani; na kama vile Mordekai alivyoamuru, Wayahudi wakaandikiwa, pamoja na maakida na maliwali, na wakuu wa majimbo toka Bara Hindi mpaka Kushi, majimbo mia na ishirini na saba, kila jimbo kwa mwandiko wake, na kila taifa kwa lugha yake; na Wayahudi kwa mwandiko wao na kwa lugha yao. Akaandika kwa jina la mfalme Ahasuero, na kutia muhuri kwa pete ya mfalme, akazipeleka barua kwa matarishi, wamepanda farasi, wamepanda wanyama wepesi sana waliotumika kwa huduma ya mfalme, ndio waliozalishwa katika zizi la mfalme. Katika barua hizo mfalme aliwaruhusu Wayahudi wakusanyike katika kila mji na kuzisimamia maisha zao, kuangamiza, na kuua, na kulifisha jeshi lote la watu na la jimbo watakaowaondokea, wao na wadogo wao na wanawake; na kuyachukua mali yao kuwa nyara;”

Mungu alimfufua Yesu Kristo ambaye wazee walimshulubisha wakidhani ya kuwa wamemaliza hatima yake, walipomuua waliomba kwamba kaburi lake lilindwe na likawekwa na muhuri kuwa lisibadilike neno lolote katika kile ambacho kimeagizwa na askari waliwekwa kulinda lakini Yesu alifufuka siku ya tatu!

Matendo 3:14-18 “Bali ninyi mlimkana yule Mtakatifu, yule Mwenye haki, mkataka mpewe mwuaji; mkamwua yule Mkuu wa uzima, ambaye Mungu amemfufua katika wafu; na sisi tu mashahidi wake. Na kwa imani katika Jina Lake, jina lake limemtia nguvu mtu huyu mnayemwona na kumjua; na imani ile iliyo kwake yeye imempatia huyu uzima huu mkamilifu mbele yenu ninyi nyote. Basi sasa, ndugu, najua ya kuwa mliyatenda haya kwa kutokujua kwenu, kama na wakuu wenu walivyotenda. Lakini mambo yale aliyohubiri Mungu tangu zamani kwa kinywa cha manabii wake wote, ya kwamba Kristo wake atateswa, ameyatimiza hivyo.”

Mungu yule yule ambaye alibadilisha historia za watau wake hapo juu anauwezo wa kubadilisha historia yako, Mungu anaposhika kalamu anafungua ukurasa mpya katika maisha yako  na kusababisha kitu kipya katika maisha yako kitokee, haijalishi unapitia katika mapito gani, Wanadamu wote walikuwa wameandikiwa kifo na laana ya dhambi lakini kupitia kazi iliyofanywa na Bwana wetu Yesu Kristo pale msalabani Yesu amekuandikia habari mpya , ameifuta ile hati iliyoandikwa ya sheria iliyokuwa na shuhuda zetu na kesi iliyokuwa inatukabili ameigongomelea msalabani isiwepo tena ile hati ya kutuhukumu imefutwa, Mungu anaweza kukufanya kuwa kiumbe kipya leo kama uliandikiwa hukumu hati ya hukumu imefutwa, kama uliandikwa katika kitabu cha hukumu mambo yako ya kale yamepita na yamekuwa mapya leo, haijalishi wanadamu wamekusudia nini leo katika maisha yako nakuletea Yesu Kristo mzima mzima ambaye atayabadilisha maisha yako na kuyafanya upya, wale waliokuzomea na kukuandalia kaburi, wale waliokushitaki na kukuandikia hukumu, Yesu anabadilisha maisha yako anabadili hatima yako, hakuna mwanadamu mwenye hati miliki ya Mungu, Mungu ni wa wote ni Mungu wa wote wenye mwili, na Mungu akiishika kalamu na hubadili maisha yako kabisa na kukupa muelekeo mpya, Mungu anaposhika kalamu ndugu yangu kila kitu kitakuwa kipya tofauti na matarajio yako, Mungu anaposhika kalamu hakuna historia mbovu isiyoweza kubadilishwa, hakuna aliyechelewa sana asiyeweza kusawazishiwa, hakuna aliye na doa kubwa lisiloweza kufutika, hakuna aliyekatwa asiyeweza kuchipuliwa, hakuna aliyeachwa asiyeweza kurejezwa, Muda usingeliweza kutosha kukupa shuhuda za Ayubu ambaye shetani alifilisi kila kitu lakini Mungu aliposhika kalamu, Ayubu akawa tajiri mara mbili zaidi, Muda usingeliweza kutosha kuleta habari za Petro na Paulo na Sila ambao walitiwa gerezani na maadui zao wakitarajia kuwa watakuwa wamewaweza au kuwaweka kizuizini ili yamkini wawaangamize baadaye lakini Mungu aliposhika kalamu hali ilibadilika na mambo yakawa tofauti itakuwa hivyo pia kwako leo, katika maisha yako, katika  ndoa yako,  katika huduma yako, kwaajili ya watoto wako, kabila lako, jamii yako, taifa lako, ukoo wako, biashara zako, masomo yako, tumbo lako la uzazi na kadhalika, Ni swala la Muda tu Mungu anaposhika kalamu kila kitu huwa tofauti, waliosema hutoboi Mungu nanaposhika kalamu wataisoma namba, hakuna jambo lililogumu lisilowezekana kwa Mungu, Hatima yako iko mikononi mwa Mungu, hakuna mchawi, wala mganga wala mzimu, wale pepop, wala shetani. Wala jinni wala mtu yeyote yule anayeweza kukuandikia kinyume na kile Mungu amekiandika leo ni siku yako ya kuwekwa huru, ni siku ambayo Mungu ataweka sawa pale palipoyumba katika maisha yako Haleluyaaaa!

Dua!   

Ee Bwana mtumwa wako ninaomba! Katika jina la Yesu Kristo; nakusihi ushike kalamu sasa na kubadilisha maisha ya kila mmoja wetu na kuandika hatima mpya, andika hatima mpya ya ndugu yangu huyu, andika hatima mpya ya dada yangu huyu, andika hatima mpya ya familia zetu, andika hatima mpya ya huduma zetu, andika hatima mpya ya vizazi vyetu, andika hatima mpya ya taifa letu, andika ee Bwana tofauti na wanadamu walivyoandika, andika ee Bwana kwaajili ya jina lako tafakatifu, andika ee Bwana kupitia neema yako na upendo wako mkubhwa sana na wingi wa rehema zako tafadhali Bwana mwandikie kila mmoja wetu ukurasa mpya wenye kufaa kama ulivyokusudia toka mwanzo  namwombea kila mmoja anayesoma ujumbe huu katika jina la Mwanao Mpendwa Yesu Kristo ameeen!

Na Rev. Innocent Samuel Kamote.

Mkuu wa wajenzi mwenye Hekima!

Jumatatu, 21 Julai 2025

Je, Mungu wako anaweza kukuokoa?

 

Zaburi 34:15-18 “Macho ya Bwana huwaelekea wenye haki, Na masikio yake hukielekea kilio chao. Uso wa Bwana ni juu ya watenda mabaya, Aliondoe kumbukumbu lao duniani. Walilia, naye Bwana akasikia, Akawaponya na taabu zao zote. Bwana yu karibu nao waliovunjika moyo, Na waliopondeka roho huwaokoa.”




Utangulizi:

Mojawapo ya sifa kubwa ya Mungu aliye hai ni pamoja na kuokoa! Mungu wa kweli ni lazima awe na sifa ya kuokoa na uwezo wa kufanya hivyo, Watu wengi wanafahamu kuwa Moja ya kazi ya Mungu ni kumuokoa mwanadamu na dhambi zake pamoja na matokeo ya dhambi hizo, hata hivyo sio tu kuwa Mungu hutuokoa na dhambi na matokeo yake yaani athari zake lakini pia hutuokoa na hatari za namna mbalimbali kwa hiyo Mungu hutuokoa na hatari za aina zote. Mungu ni mwokozi.

Zaburi 68:19-22 “Na ahimidiwe Bwana, Siku kwa siku hutuchukulia mzigo wetu; Mungu ndiye wokovu wetu. Mungu kwetu sisi ni Mungu wa kuokoa; Na njia za kutoka mautini zina YEHOVA Bwana. Naam, Mungu atakipasua kichwa cha adui zake, Utosi wenye nywele wa mtu afulizaye kukosa. Bwana alisema, Kutoka Bashani nitawarudisha, Nitawarudisha kutoka vilindi vya bahari;

Kimsingi kila mwanadamu anahitaji wokovu, katika maeneo mbalimbali, Tangu anguko la Adamu katika bustani ya Edeni mambo yetu wanadamu yamekuwa hayatuendei kwa ukamilifu kama ilivyokuwa mwanzo na kwa sababu hiyo tunamuhitaji Mwokozi, maisha ya mwanadamu yamejawa na taabu na safari yetu haijanyooka, maisha yetu yamekuwa ya milima na mabonde, mchanganyiko wa huzuni na furaha, uchungu na utamu, hatuna utulivu wa kutosha hatuwezi kufurahia maisha moja kwa moja, Amani ya kweli imeingia mushikeli, fadhaa zimetuzunguka kila upande, kukikucha ni kama hatuifurahii asubuhi, hata wale tunaowaona kwa macho kuwa ni kama wanaonekana wana mafanikio makubwa wengine wana changamoto kubwa zaidi kiasi cha kuwahurumia, tunamuhitaji Mungu atakayetuokoa, tunamuhitaji atakayetuokoa mikononi mwa adui zetu ili hatimaye tumuabudu Mungu pasipo hofu!, Watu waliomcha Mungu tangu mwanzo walikuwa wakitazamia wokovu wake, walikuwa wanajua ya kuwa Mungu ameahidi kumleta kiongozi atakayekuwa na msaada Mkubwa kwa wanadamu kifurushi kamili cha wokovu kingekuwa juu yake yani huyu ni Yesu!

Luka 1:69-75 “Ametusimamishia pembe ya wokovu Katika mlango wa Daudi, mtumishi wake. Kama alivyosema tangu mwanzo Kwa kinywa cha manabii wake watakatifu;Tuokolewe na adui zetu Na mikononi mwao wote wanaotuchukia; Ili kuwatendea rehema baba zetu, Na kulikumbuka agano lake takatifu; Uapo aliomwapia Ibrahimu, baba yetu, Ya kwamba atatujalia sisi, Tuokoke mikononi mwa adui zetu, Na kumwabudu pasipo hofu, Kwa utakatifu na kwa haki Mbele zake siku zetu zote.”

Luka 2:25-31 “Na tazama, pale Yerusalemu palikuwa na mtu, jina lake Simeoni, naye ni mtu mwenye haki, mcha Mungu, akiitarajia faraja ya Israeli; na Roho Mtakatifu alikuwa juu yake. Naye alikuwa ameonywa na Roho Mtakatifu ya kwamba hataona mauti kabla ya kumwona Kristo wa Bwana. Basi akaja hekaluni ameongozwa na Roho; na wale wazazi walipomleta mtoto Yesu ndani, ili wamfanyie kama ilivyokuwa desturi ya sheria, yeye mwenyewe alimpokea mikononi mwake, akamshukuru Mungu, akisema, Sasa, Bwana, wamruhusu mtumishi wako, Kwa amani, kama ulivyosema; Kwa kuwa macho yangu yameuona wokovu wako, Uliouweka tayari machoni pa watu wote;”

Baba zetu walikuwa wakiutumainia wokovu, wokovu ambao kwa kiyunani ni “SOTERIA” ni kifurushi cha ukombozi ambacho ndani yake kuna msamaha wa dhambi, kuna ushindi dhidi ya dhambi, kuna kutokulipwa sawaswa na makosa yetu, kuna faraja na amani ya kweli, kuna kuponywa magonjwa, kuna kushindiwa vita, kuna kuokolewa kutoka utumwani, kuna nguvu ya kushinda umasikini, na kuharibiwa kwa laana zote ni nani asiye hitaji wokovu? Kila mmoja anahitaji wokovu na kwa sababu hiyo kila mmoja anamuhitaji mwokozi na ni Mungu pekee anayeweza kuokoa, wokovu ni kazi ya Mungu peke yake! Leo basi tutachukua muda kidogo kujikumbusha juu ya somo hili muhimu lenye swali Je Mungu wako aweza kukuokoa? Na tutajifunza hivyo kwa kuzingatia vipengele vitatu vifuatavyo!


·         Je Mungu wako aweza kukuokoa?

·         Mungu awezaye kuokoa!

·         Je wewe una Mungu anayeweza kuokoa?


Je Mungu wako aweza kuokoa?

Kwa kuwa wanadamu wanapitia changamoto za aina mbalimbali katika maisha! Mara nyingi sana wanadamu wamekuwa wakijiuliza swali Je Mungu anaweza kuokoa? Kwa maana ya kuwa katika kila changamoto tunazokutana nazo tunaweza kujiuliza kuwa je Mungu anaweza kunitoa katika hali hii? Je Mungu anaweza kukushindia katika hali hiyo unayoipitia? Unaweza wakati mwingine kupita katika hali na mazingira magumu sana ya kusikitisha, kutisha, kuhuzunisha, kuvunja moyo na kukatisha tamaa na ukadhani ya kuwa Mungu hashughuliki na hali hiyo au hawezi kushughulika na hali unayoipitia Je Mungu wako anaweza kukuokoa? Katika maandiko tunapewa mifano ya watu mbalimbali ambao walikuwa wanakabiliwa na hali za kutisha na katika kutishiwa huko ilifikiriwa kuwa hawataweza kabisa kupata wokovu, shetani vilevile kupitia maajenti wake alitaka kujua kuwa watu hao wataokolewa namna gani katika kona ambayo walikuwa wamekabwa? Na kutishiwa ikifikiriwa ya kuwa hakuna mungu anayeweza kuwaokoa!

Hezekia - 2Wafalme 19:10-14 “Mwambieni Hezekia, mfalme wa Yuda, maneno haya, mkisema, Asikudanganye Mungu wako unayemtumaini, akisema, Yerusalemu hautatiwa katika mikono ya mfalme wa Ashuru. Tazama, umesikia ni mambo gani wafalme wa Ashuru waliyozitenda nchi zote, kwa kuziangamiza kabisa; je! Utaokoka wewe? Je! Miungu ya mataifa wale, ambao baba zangu waliwaangamiza, imewaokoa? Yaani, Gozani, na Harani, na Resefu, na wana wa Adini waliokuwa katika Telasari? Yuko wapi mfalme wa Hamathi, na mfalme wa Arpadi, na mfalme wa mji wa Sefarvaimu, na wa Hena, na wa Iva? Basi Hezekia akaupokea waraka katika mikono ya wale wajumbe, akausoma; kisha Hezekia akapanda, akaingia katika nyumba ya Bwana, akaukunjua mbele za Bwana.”

Shadraka, Meshaki na Abednego - Daniel 3:13-15 “Basi Nebukadreza akatoa amri kwa hasira na ghadhabu, waletwe hao Shadraka, na Meshaki, na Abednego. Basi wakawaleta watu hao mbele ya mfalme. Nebukadreza akajibu, akawaambia, Enyi Shadraka, na Meshaki, na Abednego, je! Ni kwa makusudi hata hammtumikii mungu wangu wala kuisujudia sanamu ya dhahabu niliyoisimamisha? Basi sasa, kama mkiwa tayari wakati mtakapoisikia sauti ya panda, na filimbi, na kinubi, na zeze, na santuri, na zomari, na namna zote za ngoma, kuanguka na kuisujudia sanamu niliyoisimamisha, ni vema; bali msipoisujudia, mtatupwa saa iyo hiyo katika tanuru iwakayo moto; naye ni nani Mungu yule atakayewaokoa ninyi na mikono yangu?

Daniel - Daniel 6:19-20 “Asubuhi mfalme akaondoka mapema, akaenda kwa haraka mpaka penye lile tundu la simba. Naye alipolikaribia lile tundu, akamlilia Danieli kwa sauti ya huzuni; mfalme akanena; akamwambia Danieli, Ee Danieli, mtumishi wa Mungu aliye hai, je! Mungu wako, unayemtumikia daima, aweza kukuponya na simba hawa?

Hezekia, Shadraki Meshaki na Abednego pamoja na Daniel katika nyakati tofauti waliwahi kuwa na wakati Mgumu ambao ulihitaji, wokovu na kila wakati walioupitia walipaswa kuonyesha kama Mungu wanayemuamini anaweza kuwaokoa, zilikuwa ni nyakati ngumu kwani ni mpaka uwe na imani katika Mungu wa kweli, anayeweza kuokoa ili uweze kupita katika hali hiyo!, Wapinzani wako na wale wanaokupa changamoto za Mungu uliye naye wanataka tu kujua kuwa katika hali uliyoko je Mungu wako anaweza kukuokoa? Watataka kuona kama Mungu wako anaweza kukusaidia kama unamwamini Mungu wa kweli Muumba wa mbingu na ardhi kwa hakika yeye anaweza kuokoa!

Yesu Kristo alipokuwa ameshitakiwa kwa husuda na kuhukumiwa kuuawa msalabani adui zake walimsanifu wakitaka ashuke msalabani ili yamkini ikiwezekana nao waweze kumuamini, alipolia Mungu wangu Mungu wangu mbina umeniacha, walimdhihaki wakisema anamuita Mungu aje kumuokoa walidhani kuwa Msalaba ni hatua ya mwisho na ya kuwa kama wamemtundika msalabani hawezi kuchomoka tena, walisema amemtegemea Mungu na amwokoe sasa!  

Mathayo 27:39-43 “Nao waliokuwa wakipita njiani wakamtukana, wakitikisa-tikisa vichwa vyao, wakisema, Ewe mwenye kulivunja hekalu na kulijenga kwa siku tatu, jiokoe nafsi yako; ukiwa ndiwe Mwana wa Mungu, shuka msalabani. Kadhalika na wale wakuu wa makuhani wakamdhihaki pamoja na waandishi na wazee, wakisema, Aliokoa wengine, hawezi kujiokoa mwenyewe.Yeye ni mfalme wa Israeli; na ashuke sasa msalabani, nasi tutamwamini. Amemtegemea Mungu; na amwokoe sasa, kama anamtaka; kwa maana alisema, Mimi ni Mwana wa Mungu.”

Wakati mwingine adui atakuweka mahali ambapo anadhani kwamba huwezi kuchomoka na ya kuwa hata Mungu unayemuamini hawezi kukuokoa na atakuchungulia na kukudhihaki akifikiri ya kuwa hakuna anayeweza kukuokoa, Lakini jambo moja la kufurahia ni kuwa kama unamwamini Mungu aliye hai tambua ya kuwa Mungu mwenyezi, Mungu wa baba zetu Mungu wa Ibrahimu, na Isaka na Yakobo ni mwokozi na hatashindwa kukuokoa hata kidogo, Imeandikwa hatamwacha mtakatifu wake aone uharibifu, Mungu hatatuacha katika uharibifu hata kidogo! Atakuokoa yeye ni mwokozi!


Mungu awezaye kuokoa!

Mungu anayeweza kuokoa ni yule ambaye anaweza kumuokoa mtu au taifa au jamii katika shida zao zote, Ni Mungu ambaye hawezi kuvumilia mateso na huzuni, Ni Mungu anayeweza kukuepusha na majanga ya kila aina, majaribu ya kila aina na mateso ya kila aina, matisho ya kila aina, mitego ya kila aina, Magonjwa ya kila aina, hatari za kila aina na hata kifo, sio tu kuwa Mungu anaweza kuokoa lakini vile vile anauwezo wa kulinda na hata kuingilia kati maswala mbalimbali yanayoonekana kuwa magumu katika maisha yetu.Yeye anatujua vema wakati tunapohitaji msaada wake na hujitokeza mara na kuuleta wokovu kwa wakati anajua muda na wakati sahihi wa kukutetea na kufanya hivyo:-

Wakati Hezekia alipokuwa akitishiwa kuhusu mji wa Yerusalem kuwa utapigwa na Ashuru na kupewa shuhuda jinsi mfalme wa Ashuru alivyoangamiza miji mingine na miungu, hata kuandikiwa barua ya vitisho yeye aliichukua barua hiyo na kuipeleka mbele za Mungu wake hekaluni na kisha akaishitakia mbele za Bwana Mungu wake awezaye kuokoa, katika namna ya kushangaza sana Mungu aliyajibu maombi yake na hali ya mambo ikawa tofauti, Mungu alimuokoa Hezekia na watu wake na mji wa Yerusalem lakini pia Senekarebu mfalme wa Ashuru aliuawa mbele ya mungu wake asiye na msaada.

2Wafalme 19:15-19 “Naye Hezekia akaomba mbele za Bwana, akasema, Ee Bwana, Mungu wa Israeli, ukaaye juu ya makerubi, wewe, naam, wewe peke yako, ndiwe Mungu wa falme zote za dunia; wewe ndiwe uliyeziumba mbingu na nchi. Tega sikio lako, Ee Bwana, usikie; fumbua macho yako, Ee Bwana, uone; uyasikie maneno ya Senakeribu, ambayo amemtuma mtu aje nayo ili kumtukana Mungu aliye hai. Ni kweli, Bwana, wafalme wa Ashuru wamewaharibu mataifa na nchi zao, na kuitupa miungu yao motoni; kwa maana haikuwa miungu, bali ni kazi ya mikono ya wanadamu; ilikuwa miti na mawe tu, ndiyo sababu wakaiharibu. Basi sasa, Ee Bwana, Mungu wetu, utuokoe na mkono wake, nakusihi, ili kwamba falme zote za dunia zipate kujua ya kuwa wewe ndiwe Bwana Mungu, wewe peke yako.”

2Wafalme 19:32-37 “Basi Bwana asema hivi katika habari za mfalme wa Ashuru, Yeye hatauingia mji huu, wala hatapiga mshale hapa, wala hatakuja mbele yake kwa ngao, wala hatajenga boma juu yake. Njia ile ile aliyojia, kwa njia iyo hiyo atarudi zake, wala hataingia ndani ya mji huu, asema Bwana. Maana nitaulinda mji huu, niuokoe, kwa ajili yangu mwenyewe, na kwa ajili ya Daudi, mtumishi wangu. Ikawa usiku uo huo malaika wa Bwana alitoka, akakiingia kituo cha Waashuri, akawapiga watu mia na themanini na tano elfu. Na watu walipoondoka asubuhi na mapema, kumbe! Hao walikuwa maiti wote pia. Basi Senakeribu mfalme wa Ashuru akaondoka, akaenda zake, akarudi akakaa Ninawi. Ikawa, alipokuwa akiabudu nyumbani mwa Nisroki, mungu wake, Adrameleki na Shareza wakampiga kwa upanga; wakaikimbilia nchi ya Ararati. Na Esar-hadoni mwanawe akatawala mahali pake.”

Wakati Daniel alipofanyiwa fitina na mawaziri wenye wivu kiasi cha Daniel kutupwa katika tundu la simba wenye njaa, jambo la kushangaza ni kuwa wakati mfalme alipojaribisha kuwatupa wale waliofanya fitina katika tundu la simba ni ukweli ulio wazi kuwa walitafunwa juu juu hata kabla miili yao haijagusa chini na tangu wakati huo mfalme aliamuru watu wote katika utawala wake wamuabudu na kumtumikia Mungu wa Daniel kwa sababu ni Mungu aliye hai na mwenye uweza wa kuokoa!

Daniel 6:21-27 “Ndipo Danieli akamwambia mfalme, Ee mfalme, uishi milele. Mungu wangu amemtuma malaika wake, naye ameyafumba makanwa ya simba, nao hawakunidhuru; kwa kuwa mbele zake mimi nalionekana kuwa sina hatia; tena, mbele yako, Ee mfalme, sikukosa neno. Basi mfalme akafurahi sana, akaamuru wamtoe Danieli katika lile tundu. Ndipo Danieli akatolewa katika lile tundu, wala dhara lo lote halikuonekana mwilini mwake, kwa sababu alikuwa anamtumaini Mungu wake. Mfalme akaamuru, nao wakawaleta wale watu waliomshitaki Danieli, wakawatupa katika tundu la simba, wao, na watoto wao, na wake zao; na wale simba wakawashinda wakaivunja mifupa yao vipande vipande, kabla hawajafika chini ya tundu. Ndipo mfalme Dario akawaandikia watu wa kabila zote, na taifa zote, na lugha zote, waliokaa juu ya uso wa dunia; Amani na iongezeke kwenu. Mimi naweka amri, ya kwamba katika mamlaka yote ya ufalme wangu watu watetemeke na kuogopa mbele za Mungu wa Danieli; maana yeye ndiye Mungu aliye hai, adumuye milele, na ufalme wake ni ufalme usioharibika, na mamlaka yake itadumu hata mwisho. Yeye huponya na kuokoa, hutenda ishara na maajabu mbinguni na duniani, ndiye aliyemponya Danieli na nguvu za simba.”

Wakati Shadraka na Meshaki na Abednego walipotupwa katika tanuru la moto uliokolezwa sana huku mfalme Nebukadreza akidhania ya kuwa hakuna Mungu anayeweza kuwaokoa ni ukweli uliowazi kuwa vijana hao wa kiyahudi walimuamini Mungu aliye hai na hata walipotupwa kwenye moto muujiza mkubwa ulitokea kwani walikuwa akipiga stori na malaika kwenye moto wakiwa salama bila kuungua tukio na mujiza uliopelekea mfalme kuamuru kuwa watu wote wamuabudu Mungu aliyeweza kuwaokoa watu wake katika tanuru la Moto kwa sababu hakuonekana Mungu anayeweza kuokoa kwa namna kama ile.

Daniel 3:19-29 “Ndipo Nebukadreza akajaa ghadhabu, na sura ya uso wake ikabadilika juu ya Shadraka, na Meshaki, na Abednego, basi akatoa amri watie moto ile tanuru mara saba kuliko desturi yake ya kutiwa moto. Kisha akawaamuru baadhi ya watu mashujaa wa jeshi lake kuwafunga Shadraka, na Meshaki, na Abednego, na kuwatupa katika ile tanuru iliyokuwa ikiwaka moto. Basi watu hao wakafungwa, hali wamevaa suruali zao, na kanzu zao, na joho zao, na mavazi yao mengine, wakatupwa katikati ya ile tanuru iliyokuwa ikiwaka moto. Basi kwa sababu amri ya mfalme ilikuwa ni kali, na ile tanuru ilikuwa ina moto sana, mwako wa ule moto ukawaua wale watu waliowashika Shadraka, na Meshaki, na Abednego. Na watu hao watatu, Shadraka, na Meshaki, na Abednego, wakaanguka, hali wamefungwa, katikati ya ile tanuru iliyokuwa inawaka moto. Ndipo Nebukadreza akastaajabu, akainuka kwa haraka; akanena, akawaambia mawaziri wake, Je! Hatukutupa watu watatu, hali wamefungwa, katikati ya moto? Wakajibu, wakamwambia mfalme, Kweli, Ee mfalme. Akajibu, akasema, Tazama, mimi naona watu wanne, nao wamefunguliwa, wanatembea katikati ya moto hali hawana dhara; na sura yake yule wa nne ni mfano wa mwana wa miungu. Kisha Nebukadreza akaukaribia mdomo wa ile tanuru iliyokuwa inawaka moto. Akanena, akasema, Enyi Shadraka, na Meshaki, na Abednego, watumishi wa Mungu Aliye juu, tokeni, mje huku. Ndipo Shadraka, na Meshaki, na Abednego, wakatoka katika ule moto. Na maamiri, na manaibu, na maliwali, na mawaziri, waliokuwa wamekusanyika pamoja, wakawaona watu hao, ya kuwa ule moto ulikuwa hauna nguvu juu ya miili yao, wala nywele za vichwa vyao hazikuteketea, wala suruali zao hazikubadilika, wala harufu ya moto haikuwapata hata kidogo. Nebukadreza akanena, akasema, Na ahimidiwe Mungu wa Shadraka, na Meshaki, na Abednego; aliyemtuma malaika wake, akawaokoa watumishi wake waliomtumaini, wakaligeuza neno la mfalme, na kujitoa miili yao ili wasimtumikie mungu mwingine, wala kumwabudu, ila Mungu wao wenyewe. Basi mimi naweka amri ya kuwa kila kabila ya watu, na kila taifa, na kila lugha, watakaonena neno lo lote lisilopasa juu ya huyo Mungu wa Shadraka, na Meshaki, na Abednego, watakatwa vipande vipande, na nyumba zao zitafanywa jaa; kwa kuwa hakuna Mungu mwingine awezaye kuokoa namna hii.”

Yesu Kristo ambaye alidhihakiwa na kusulubiwa msalabani na kusanifiwa na adui zake na kupewa maneno ya kejeli walidhani ya kuwa Mungu hawezi kumsaidia, Neno la Mungu linasema, Mungu alimsikiliza na alimuokoa na mauti na hakumwacha Mtakatifu wake aone uharibifu kwani Kristo Yesu huyo Mungu alimfufua

Matendo 2:32 “Basi kwa kuwa ni nabii, akijua ya kuwa Mungu amemwapia kwa kiapo, ya kwamba katika uzao wa viuno vyake atamketisha mmoja katika kiti chake cha enzi; yeye mwenyewe akitangulia kuyaona haya, alitaja habari za kufufuka kwake Kristo, ya kwamba roho yake haikuachwa kuzimu, wala mwili wake haukuona uharibifu. Yesu huyo Mungu alimfufua, na sisi sote tu mashahidi wake.”

Matendo 4:9-12 “kama tukiulizwa leo habari ya jambo jema alilofanyiwa yule mtu dhaifu, jinsi alivyoponywa, jueni ninyi nyote na watu wote wa Israeli ya kuwa kwa jina la Yesu Kristo wa Nazareti, ambaye ninyi mlimsulibisha, na Mungu akamfufua katika wafu, kwa jina hilo mtu huyu anasimama ali mzima mbele yenu. Yeye ndiye jiwe lile lililodharauliwa na ninyi waashi, nalo limewekwa kuwa jiwe kuu la pembeni. Wala hakuna wokovu katika mwingine awaye yote, kwa maana hapana jina jingine chini ya mbingu walilopewa wanadamu litupasalo sisi kuokolewa kwalo.”      

                          

Je wewe una Mungu anayeweza kuokoa?

Tumejifunza kutoka katika mifano ya kibiblia ya wenzetu ambao walikuwa na Mungu anayeweza kuokoa na aliwaokoa walipokuwa na changamoto za aina mbalimbali, ukiwa na Mungu mwenye nguvu na anayeweza kuokoa unaweza kutembea katika hii dunia ukiwa na Amani na furaha na kiburi ya kuwa una Mungu anayeweza kutumainiwa, Mungu anayeweza kutegemewa, Mungu aliye hai, Mungu anayetetea, Mungu anayejali, Mungu anayelinda, Mungu anayejishughulisha sana na Mambo yetu, ukiwa na Mungu wa aina hii ni raha iliyoje duniani. Watakatifu waliotutangulia walikuwa na Mungu wa aina hii anayeweza kuokoa na waliufurahia wokovu wao katika mazingira na maeneo mbalimbali ni Mungu wa pekee anayeweza kutumainiwa ni yeye peke yake anayeokoa, Mungu mwenyewe amejifunua kwetu na kutamba kuwa anaweza kuokoa na kuwa hakuna Mungu mwingine

Isaya 43:11-15 “Mimi, naam, mimi, ni Bwana, zaidi yangu mimi hapana mwokozi. Nimetangaza habari, nimeokoa, nimeonyesha, na hapakuwa mungu wa kigeni kati yenu; kwa sababu hiyo ninyi ni mashahidi wangu, asema Bwana, nami ni Mungu. Naam, tangu siku ya leo, mimi ndiye; wala hapana awezaye kuokoa katika mkono wangu; mimi nitatenda kazi, naye ni nani awezaye kuizuia? Bwana, Mkombozi wenu, Mtakatifu wa Israeli, asema hivi; Kwa ajili yenu nimetuma ujumbe Babeli nami nitawashusha wote mfano wa wakimbizi, naam, Wakaldayo, katika merikebu zao walizozifurahia. Mimi ni Bwana, Mtakatifu wenu, Muumba wa Israeli, mfalme wenu.”

Sisi wakristo tunamuamini Mungu anayeweza kutuokoa na hakuna mwingine duniani wala mbinguni awezaye kuokoa isipokuwa yeye peke yake na kwa jina lake Yesu Kristo ukiliitia Mungu amekusudia kutupa wokovu kwa yeye, kila mmoja anapaswa kujitathimini kama je kweli ana Mungu anayeweza kuokoa? Mimi ninaye Mungu anayeweza kuokoa, sisi tunaye Mungu anayeweza kuokoa, Maandiko yanamtaja Yesu, kuwa ni Yesu Peke yake mwenye uwezo huo! Nje ya Yesu hakuna mwokozi

Matendo 4:10-12 “jueni ninyi nyote na watu wote wa Israeli ya kuwa kwa jina la Yesu Kristo wa Nazareti, ambaye ninyi mlimsulibisha, na Mungu akamfufua katika wafu, kwa jina hilo mtu huyu anasimama ali mzima mbele yenu. Yeye ndiye jiwe lile lililodharauliwa na ninyi waashi, nalo limewekwa kuwa jiwe kuu la pembeni. Wala hakuna wokovu katika mwingine awaye yote, kwa maana hapana jina jingine chini ya mbingu walilopewa wanadamu litupasalo sisi kuokolewa kwalo.”

Waebrania 7:25-27 “Naye, kwa sababu hii, aweza kuwaokoa kabisa wao wamjiao Mungu kwa yeye; maana yu hai sikuzote ili awaombee. Maana ilitupasa sisi tuwe na kuhani mkuu wa namna hii aliye mtakatifu, asiyekuwa na uovu, asiyekuwa na waa lo lote, aliyetengwa na wakosaji, aliyekuwa juu kuliko mbingu; ambaye hana haja kila siku, mfano wa wale makuhani wakuu wengine, kwanza kutoa dhabihu kwa ajili ya dhambi zake mwenyewe, kisha kwa ajili ya dhambi za hao watu; maana yeye alifanya hivi mara moja, alipojitoa nafsi yake.”

Je wewe unaye Mungu anayeweza kukuokoa? Shida na changamaoto zako hazikomi wala haziondoki kwa sababu huna Mungu anayeweza kuokoa, huna Mungu anayeweza kukusikia wala huna Mungu anayeshughulika na mambo yako, Mungu asiye na msaada ni wa nini? je wewe una Mungu wa aina gani? Sisi Mungu wetu yuko hai, yuko mbinguni na uwezo anao alitakalo hulitenda.Na ni kimbilio letu

Zaburi 115:3-9 “Lakini Mungu wetu yuko mbinguni, Alitakalo lote amelitenda. Sanamu zao ni fedha na dhahabu, Kazi ya mikono ya wanadamu. Zina vinywa lakini hazisemi, Zina macho lakini hazioni, Zina masikio lakini hazisikii, Zina pua lakini hazisikii harufu, Mikono lakini hazishiki, miguu lakini haziendi, Wala hazitoi sauti kwa koo zake. Wazifanyao watafanana nazo, Kila mmoja anayezitumainia. Enyi Israeli, mtumainini Bwana; Yeye ni msaada wao na ngao yao.”

Zaburi 46:1-5 “Mungu kwetu sisi ni kimbilio na nguvu, Msaada utakaoonekana tele wakati wa mateso. Kwa hiyo hatutaogopa ijapobadilika nchi, Ijapotetemeka milima moyoni mwa bahari. Maji yake yajapovuma na kuumuka, Ijapopepesuka milima kwa kiburi chake. Kuna mto, vijito vyake vyaufurahisha mji wa Mungu, Patakatifu pa maskani zake Aliye juu. Mungu yu katikati yake hautatetemeshwa; Mungu atausaidia asubuhi na mapema.”

Nakutangazia ya kuwa mimi nina Mungu aliye hai, nina shuhudua nyingi za ajabu na za kutisha jinsi na namna Mungu aliye hai aliyonishindia na kunipigania, Ikiwa unataka kuona uhai wa Mungu wangu wewe jaribu kushughulika nami na ujichanganye unikorofishe katika habari za Mungu wangu, I tell you the truth you will be eliminated! Do tot mess up with me or my God! Kama unataka kupotea chezea mimi cheza na Mungu wangu ni Mungu ambaye anaokoa na kubariki na ameahidi sio tu kunibariki lakini pia yeye ni ngao yangu na thawabu yangu kubwa sana ninakusihi msomaji wangu na msikilizaji wangu hakikisha ya kuwa una uhusiano na Mungu aliye hai Mungu wa kweli na hutakuja kujuta. Yeyote atakaye jaribu kushindana nawe atasambaratishwa vibaya, ni Mungu ambaye haruhusu uonevu hata kidogo, haogopi wafalme wala mtu mwonevu wote anawakemea kwa sababu ya aina ya mafuta aliyokupaka onja habari za Bwana Mungu wangu utembee kifua mbele Mwamini Bwana Yesu utetewe, Mwamini mfanye kuwa Bwana na mwokozi wa maisha yako na utaokolewa onja uone ya kuwa Bwana ni mwema! Yesu Kristo hana mzaha na mali yake ikiwa unamuamini na kumtegemea jua ya kuwa kwa jina lake Mungu ameruhusu watu wote waokolewe kila atakayeliitia jina la Bwana yaani Yesu Kristo ataokoka, Ni vema kumtegemea Mungu ambaye ni mwokozi, acha kutegemea miungu mingine isiyokuwa na msaada, sisi tunaye Mungu anayeokoa leo hii kama utamuamini na kumsadiki na kutegemea kwa hakika hutatahayarika, kama ilivyoandikwa ya kuwa kila amuaminiye yeye hatatatahayarika kamwe, Mungu na akuokoe katika kila changamoto unayoipitia katika jina la Yesu Kristo mwana wa Mungu aliye hai amen!

Na Rev. Innocent Samuel Kamote

Mkuu wa wajenzi mwenye Hekima 

Jumapili, 13 Julai 2025

Asizimie moyo mtu!


1Samuel 17:32-36 “Daudi akamwambia Sauli, Asizimie moyo mtu ye yote kwa ajili ya huyu; mimi mtumishi wako nitakwenda kupigana na Mfilisti huyu. Sauli akamwambia Daudi, Huwezi wewe kumwendea Mfilisti huyu upigane naye; maana wewe u kijana tu; na huyu ni mtu wa vita tangu ujana wake. Daudi akamwambia Sauli, Mtumishi wako alikuwa akichunga kondoo za baba yake, na alipokuwa akija simba, au dubu, akamkamata mwana-kondoo wa lile kundi, mimi hutoka nikamfuata, nikampiga, nikampokonya kinywani mwake; na akinirukia, humshika ndevu zake, nikampiga, nikamwua. Mtumishi wako alimwua simba na dubu pia; na huyu Mfilisti asiyetahiriwa atakuwa kama mmoja wao, kwa sababu amewatukana majeshi ya Mungu aliye hai.”


Utangulizi:

Ni muhimu kufahamu kuwa katika maisha haya mara nyingi mimi na wewe kama wanadamu huwa tunakutana na changamoto mbali mbali ambazo nyinginezo zinaweza kutuvunja moyo na kutukatisha tamaa, sio hivyo tu pia zinaweza kutuogopesha na kutufanya tupoteze kujiamini au hata kuamini kuwa Mungu anaweza kutusaidia tena, Katika Israel wakati fulani waliwahi kukutana na hali kama hii unayoipitia wewe, walikuwa katika vita na wafilisti, na katika jeshi la wafilisti alijitokeza mtu mmoja mkubwa sana mwenye nguvu na mwenye kutisha ambaye alizungumza maneno ya propaganda za kivita na kuwatia hofu sana wana wa Israel kiasi ambacho jeshi lote la Israel wakiongozwa na Sauli mfalme wao waliogopa na kuzimia moyo, Neno “Asizimie” katika Lugha ya kiebrania linasomeka kama “Nâphal” ambalo kwa kiingereza ni “fall” limetumika hivyo mara 318 likimaanisha kuanguka, au kupoteza matumaini, au kushuka chini kutoka katika hali yake ya awali, kwa Kiswahili kuvunjika moyo yaani asivunjike moyo mtu awaye yote  unapokutana na changamoto.

1Samuel 17:1-11 “Wakati huo Wafilisti walikusanya majeshi yao kwa vita, nao wakakusanyika huko Soko, ulio mji wa Yuda, wakatua kati ya Soko na Azeka, katika Efes-damimu. Naye Sauli na watu wa Israeli wakakusanyika, wakatua katika bonde la Ela, nao wakapanga vita juu ya hao Wafilisti. Wafilisti wakasimama juu ya mlima upande huu, na Waisraeli wakasimama juu ya mlima upande huu, napo palikuwa na hilo bonde katikati. Ndipo akatoka shujaa katika kambi ya Wafilisti, aliyeitwa Goliathi, wa Gathi, ambaye urefu wake ulikuwa mikono sita na shibiri moja. Alikuwa na chapeo ya shaba kichwani, tena amevaa darii ya shaba; na uzani wake ile darii ya shaba ulikuwa shekeli elfu tano za shaba. Tena amevaa mabamba ya shaba miguuni mwake, naye alikuwa na mkuki wa shaba kati ya mabega; yake. Na mti wa fumo lake ulikuwa kama mti wa mfumaji; na kichwa cha mkuki wake kilikuwa shekeli mia sita za chuma uzito wake; na mtu aliyemchukulia ngao yake akamtangulia. Naye akasimama, akawapigia kelele majeshi ya Israeli akawaambia, Mbona mmetoka kupanga vita? Je! Mimi si Mfilisti, na ninyi si watumishi wa Sauli? Jichagulieni mtu, akanishukie mimi. Kama akiweza kupigana nami na kuniua, sisi tutakuwa watumwa wenu; nami nikimshinda yeye na kumwua, ninyi mtakuwa watumwa wetu, na kututumikia. Yule Mfilisti akasema, Nayatukana leo majeshi ya Israeli; nipeni mtu tupigane. Basi Sauli na Israeli wote waliposikia maneno hayo ya Mfilisti, wakafadhaika na kuogopa sana.”

Kutokana na maneno ya shujaa huyo wa wafilisti mwenye kutisha sana Israel waliogopa na kuzimia moyo, ni jambo la kawaida wakati mwingine kwamba linapotokea jambo la kutisha kutokana na propaganda za kishetani huwa tunasahau uweza wa Mungu na ukuu wake na kuitazama ile changamoto huku tukijiuliza kama tunaweza kutokaje katika changamoto hiyo, unajiuliza nitatoboa kweli au safari hii ndio nafariki, nitatokaje katika ugonjwa huu, nawezaje kukabiliana na deni hili kubwa namna hii, aibu inakaribia, nawezaje kutoka katika matatizo haya na kwa sababu ya utisho wa hali inayotuzunguka ni rahisi kwetu kuvunjika moyo au kuzimia moyo, Kijana mdogo sana katika Israel Daudi alisimama kwa ujasiri na kuwatia moyo taifa zima ya kuwa asizimie moyo mtu! Kwani yeye atapambana na hali inayowakabili kwa jina la Mungu wa Israel!. Leo kila changamoto unayokabiliana nayo, kila ukuta unaosimama kama kikwazo katika maisha yako, kila mlima na jaribu, na mateso, na ugonjwa na majini na mapepo na nguvu za giza zinazosimama kama changamoto katika maisha yako ambazo zimekufanya ukazimia moyo kwa jina la Yesu Kristo mwana wa Mungu aliye hai tunakwenda kukabiliana nazo na kuzisambaratisha kabisa haleluyaa Asizimie moyo mtu!.Tutajifunza somo hili Asizimie Moyo mtu kwa kuzuingatia vipengele vitatu vifuatavyo:-

·         Sababu za watu kuzimia moyo!

·         Asizimie moyo mtu!

·         Kwanini asizimiye moyo mtu!

Sababu za watu kuzimia moyo!

Ni ukweli uliokuwa wazi kuwa Israel kama ilivyo kwa watu wengine walikuwa wamevunjika moyo na kuzimia kabisa kwa woga, mazingira waliokuwa wanakabiliana nayo, yalikuwa ni magumu na yenye kuogopesha sana, propaganda za kivita zilikuwa zimewatia hofu na kuwachosha, Goliath alikuwa akijitokeza kila siku asubuhi na jioni kwa siku 40 akiwatukana na kuwatisha sana, jambo lilolopelekea jeshi zima na mashujaa wakubwa wakiwepo kaka zake Daudi na mfalme Sauli kutishika na kufadhaika sana, Goliathi aliyatukana majeshi ya Israel waziwazi, hadharani kila mtu akishuhudia!

1Samuel 17:10-16 “Yule Mfilisti akasema, Nayatukana leo majeshi ya Israeli; nipeni mtu tupigane. Basi Sauli na Israeli wote waliposikia maneno hayo ya Mfilisti, wakafadhaika na kuogopa sana. Basi Daudi alikuwa mwana wa yule Mwefrathi, wa Bethlehemu ya Yuda, aliyeitwa jina lake Yese; naye huyo alikuwa na wana wanane; na yeye mwenyewe alikuwa mzee siku za Sauli, na mkongwe miongoni mwa watu. Nao wale wana watatu wa Yese waliokuwa wakubwa walikuwa wamefuatana na Sauli kwenda vitani, na majina ya hao wanawe watatu waliokwenda vitani ni haya, mzaliwa wa kwanza Eliabu, na wa pili wake Abinadabu, na wa tatu Shama. Naye huyo Daudi alikuwa mdogo wa wote; na hao watatu waliokuwa wakubwa wakafuatana na Sauli. Basi Daudi alikuwa akienda kwa Sauli na kurudi ili awalishe kondoo za baba yake huko Bethlehemu. Naye yule Mfilisti hukaribia asubuhi na jioni, akajitokeza siku arobaini.”

Sisi nasi katika maisha yetu tunaweza kufadhaika na kutishika na hata kuvunjika moyo kutokana na uhalisia wa changamoto, ni ukweli uliokuwa wazi kuwa Golitahi lilikuwa jitu kubwa lenye nguvu na uzoefu wa kivita, na jeshi lote la Israel lilimuogopa, yako mambo ambayo yakikupata wewe mwenyewe na hata wataalamu wanaweza kukubaliana kuwa ni jambo zito na kubwa, ikiwa una ukimwi, ikiwa una sukari, ikiwa umepatwa na kiharusi, ikiwa una kansa ya damu, ikiwa una changamoto ya ini, kansa, figo, changamoto za mfumo wa fahamu, umeme katika mwili, moyo na kadhalika ni magonjwa ya kutisha ambayo hata wataalamu wa afya wenyewe wanayaogopa na una historia yake namna na jinsi yalivyoua watu mbalimbali kwenye jamii yako, familia yako na hata majirani, changamoto za mikopo umiza, madeni ya aibu, kufilisika, hasara za namna mbalimbali, kutapeliwa fedha nyingi, kuporomoka kwa biashara, hali mbaya ya kiuchumi, kutokujitosheleza kwa mahitaji mbalimbali na umasikini wa kutisha vinaweza kuwa sababu ya kuzimia moyo, Sio hivyo tu maneno unayoyasikia kutoka upande wa upinzani au wa adui yako na wakati mwingine wanaweza hata kusema kuhusu Mungu wako kwamba tuone kama Mungu wake anaweza kumsaidia hivyo vyote vinaweza kukufanya ukazimia moyo, wakati unapokuwa katika changamoto kali na ngumu sana maneno ya adui zako yanaweza kukuumiza sana, na hata maneno ya wale watu usiowatarajia, kama wapendwa wenzetu, Yesu alipokuwa msalabani adui zale walisema pia kuhusu Mungu kwamba amemtegemea Mungu na amwokoe sasa Msalabani nasi tutamwamini maneno ya kuumiza!

Mathayo 27:40-43. “Ewe mwenye kulivunja hekalu na kulijenga kwa siku tatu, jiokoe nafsi yako; ukiwa ndiwe Mwana wa Mungu, shuka msalabani.Kadhalika na wale wakuu wa makuhani wakamdhihaki pamoja na waandishi na wazee, wakisema, Aliokoa wengine, hawezi kujiokoa mwenyewe. Yeye ni mfalme wa Israeli; na ashuke sasa msalabani, nasi tutamwamini. Amemtegemea Mungu; na amwokoe sasa, kama anamtaka; kwa maana alisema, Mimi ni Mwana wa Mungu.”

Hatupaswi kamwe kukosa imani na kuvunjika moyo au kuzimia moyo wala kuyatazama mazingira na badala yake tunapaswa kumwangalia Mungu ambaye ni mkubwa kuliko changamoto yako, Daudi kamwe hakukubali kuwa na aibu ya kitaifa na wala hakukubali Mungu wake adhalilike na ndugu zake waaibike, akiwa amejaaa Imani, uzoefu, ujuzi kuhusu Mungu na ujasiri mkubwa ambao wengi walikuwa wameupoteza yeye alisema atapambana na hali hiyo na kwa sababu hiyo asizimie moyo mtu, usizimie moyo kwaajili ya ugonjwa wako, usizimie moyo kwaajili ya adui zako, usizimie moyo kwaajili ya umasikini wako, usizimie moyo kwaajili ya changamoto na matatizo ya kifamilia, haijalishi adui anatisha kwa kiwango gani sisi tutamjia kwa jina la Bwana Mungu wa Israel aliye hai.

Asizimie moyo mtu!

Wakati kila mtu akiwa ameingiwa na hofu fadhaa na kukata tamaa au kuzimia Moyo, Daudi alikuwa na mtazamo tofauti na wengine Yeye alikuwa amejifunza kuwa Mungu ni mkubwa kuliko changamoto ya aina yoyote ile, alikuwa amejifunza na kupata uzoefu na shuhuda namna na jinsi Mungu alivyompa ushindi dhidi ya  wanyama wakali wenye nguvu kuliko binadamu wanyama kama Dubu, Simba na kadhalika alitambua kuwa Mungu alikuwa pamoja naye hata alipokuwa akiwachunga kondoo wa baba yake na kwa sababu hiyo Golitahi kwake lilikuwa ni jambo dogo sana wala sio la kufadhaisha mtu na hivyo aliwapa tumani watu wote pamoja na mfalme Asizimie moyo mtu!

1Samuel 17:34-37 “Daudi akamwambia Sauli, Mtumishi wako alikuwa akichunga kondoo za baba yake, na alipokuwa akija simba, au dubu, akamkamata mwana-kondoo wa lile kundi, mimi hutoka nikamfuata, nikampiga, nikampokonya kinywani mwake; na akinirukia, humshika ndevu zake, nikampiga, nikamwua. Mtumishi wako alimwua simba na dubu pia; na huyu Mfilisti asiyetahiriwa atakuwa kama mmoja wao, kwa sababu amewatukana majeshi ya Mungu aliye hai. Daudi akasema, Bwana aliyeniokoa na makucha ya simba, na makucha ya dubu, ataniokoa na mkono wa Mfilisti huyu. Sauli akamwambia Daudi, Enenda, na Bwana atakuwa pamoja nawe.”

Daudi aliamini kuwa sio kwa nguvu za kibinadamu atamkabili Goliath lakini ni kwa nguvu za Mungu na kwa msaada wa Mungu, alikumbuka shuhuda za ukuu wa Mungu na matendo yake na uaminifu wake, alitambua jinsi jina la Mungu linavyopaswa kutakaswa na kutukuzwa na alijua ya kuwa kwa jina hilo hakuna kinachoweza kusimama, alifahamu ya kuwa Mungu hawezi kutukanwa wala kudhalilishwa na jeuri na kiburi cha kibinadamu na kisha akakubali, Daudi alitambua kuwa kutukanwa kwa majeshi ya Mungu aliye hai ni kutukanwa kwa Mungu kwa hiyo alitaka kuitetea heshima ya Mungu, Daudi alitambua kuwa ushindi wake ni ushindi wa kitaifa na sio wa mtu mmoja na kuwa kushindwa kwa Goliathi ni kushindwa kwa wafilisti wote, Ni ukweli uliowazi katika ulimwengu wa roho vita ya Daudi na Goliati ilikuwa inawakilisha vita ya Yesu Kristo na Shetani, yule atakayeshindwa atakuwa mtumwa wa yule atakayeshindwa na watu wake na yule atakayeshinda atatawala yeye na watu wake kila mtu aliyeokoka ni mshindi kupitia ushindi wa Yesu Kristo, wakati Goliathi akiwa na kofia ya chuma na mabamba ya chuma kila mahali Daudi yeye hakuwa na kizuizi chochote na alikuwa na silaha laini yaani manati-kombeo na mawe matano tu laini

1Samuel 17:45-47.”Ndipo Daudi akamwambia yule Mfilisti, Wewe unanijia mimi na upanga, na fumo, na mkuki, bali mimi ninakujia wewe kwa jina la Bwana wa majeshi, Mungu wa majeshi ya Israeli uliowatukana. Siku hii ya leo Bwana atakuua mkononi mwangu, nami nitakupiga, na kukuondolea kichwa chako, nami leo nitawapa ndege wa angani na wanyama wa nchi mizoga ya majeshi ya Wafilisti, ili kwamba dunia nzima wajue ya kuwa yuko Mungu katika Israeli. Nao jamii ya watu wote pia wajue ya kwamba Bwana haokoi kwa upanga wala kwa mkuki; maana vita ni vya Bwana, naye atawatia ninyi mikononi mwetu.”

Wakati Goliathi alikuwa akitema propaganda tu na vitisho kwa kujiamini kwa kiburi na majivuno, Daudi alikuwa akizitamka shuhuda za Mungu na ukweli wa neno lake Mungu na uweza wake, ni ukweli ulio wazi kuwa siku ile Daudi alimpiga Goliathi na kwa kutumia upanga wa Goliathi mwenyewe alikata kichwa chake, tukio hili liliwapa nguvu Israel na waliwakimbiza wafilisti na kuwachinja kama walivyotaka na kujikusanyia nyara:-

1Samuel 17:48-52 “Ikawa, hapo Mfilisti alipojiinua, akaenda akamkaribia Daudi, ndipo Daudi naye akapiga mbio, akalikimbilia jeshi ili akutane na yule Mfilisti. Daudi akatia mkono wake mfukoni, akatwaa humo jiwe moja, akalitupa kwa kombeo lake, akampiga Mfilisti katika kipaji cha uso; jiwe hilo likamwingilia kipajini, akaanguka chini kifudifudi. Hivyo Daudi akamshinda yule Mfilisti kwa kombeo na jiwe, akampiga Mfilisti, akamwua; walakini Daudi hakuwa na upanga mkononi mwake. Ndipo Daudi akapiga mbio, akasimama juu ya Mfilisti, akautwaa upanga wake, akaufuta alani mwake, akamwua, akamkata kichwa kwa upanga huo. Nao Wafilisti walipoona ya kuwa shujaa wao amekufa, wakakimbia. Nao watu wa Israeli na wa Yuda wakainuka, na kupiga kelele, nao wakawafuata Wafilisti mpaka ufikapo Gathi, na mpaka malango ya Ekroni. Nao majeruhi wa Wafilisti wakaanguka kando ya njia iendayo Shaarimu, mpaka Gathi, na mpaka Ekroni.”  
           

Kwanini asizimiye moyo mtu!

Daudi alikuwa na ufahamu kuwa ushindi wake hautokani na yeye mwenyewe bali ushindi wake unatokana na Mungu, sisi nasi hatuna budi kufahamu kwamba ushindi wetu unapatikana kupitia Yesu Kristo ambaye alishinda kifo na mauti, ushindi wowote tulio nao na tutakaokuwa nao ni ushindi unaotokana na ushindi wake Kristo Yesu mwana wa Daudi.  

1Wakorintho 15:57 “Lakini Mungu na ashukuriwe atupaye kushinda kwa Bwana wetu Yesu Kristo.”

Maandiko yanatukumbusha tu kuwa hakuna changamoto kubwa kuliko Mungu wetu, kila mtu aliyeokolewa na anayemtegemea Mungu anapaswa kumtegemea Mungu na kumfanya kuwa ngao yake na kinga yake, tunapaswa kuwa na ujasiri na kuacha kupoteza matumaini, hatupaswi kamwe kuzimia moyo kama tumemfanya Bwana kuwa ngao yetu, hatupaswi kulia wala kufadhaika maana Mungu ndiye wokovu wetu, na ngome yetu na hakuna wa kutukaribia wala kutudhuru vyovyote vile!

Zaburi 27:1-3 “Bwana ni nuru yangu na wokovu wangu, Nimwogope nani? Bwana ni ngome ya uzima wangu, Nimhofu nani? Watenda mabaya waliponikaribia, Wanile nyama yangu, Watesi wangu na adui zangu, Walijikwaa wakaanguka. Jeshi lijapojipanga kupigana nami, Moyo wangu hautaogopa. Vita vijaponitokea, Hata hapo nitatumaini.”

Maandiko yanatukumbusha kuwa Mungu hutumia mambo manyonge sana, wakati ambapo Goliath anaonekana kuwa na silaha bora, mkuki mkubwa na uzoefu mkubwa vitani, huku mwili wake umezingirwa na mambamba ya shaba Daudi alikuwa ni kijana mdogo, mzuri macho mekundu lakini alijikinga kwa jina la Mungu na kumfanya Mungu kuwa tumaini lake, hii inatukumbusha kuwa Mungu anaweza kutumia chochote na kumtumia mtu yeyote bila kujali hali yake, historia yake na muonekano wake wa nje, unyonge wake au kupuuzwa kwake, Mungu hutumia vilivyodharaulika!  

1Wakorintho 1:26-29 “Maana, ndugu zangu, angalieni mwito wenu, ya kwamba si wengi wenye hekima ya mwilini, si wengi wenye nguvu, si wengi wenye cheo walioitwa; bali Mungu aliyachagua mambo mapumbavu ya dunia awaaibishe wenye hekima; tena Mungu alivichagua vitu dhaifu vya dunia ili aviaibishe vyenye nguvu; tena Mungu alivichagua vitu vinyonge vya dunia na vilivyodharauliwa, naam, vitu ambavyo haviko, ili avibatilishe vile vilivyoko; mwenye mwili awaye yote asije akajisifu mbele za Mungu.”

Maandiko yanatukumbusha kuwa Mungu ni mwaminifu na kuwa tunapokabiliana na changamoto za aina yoyote katika maisha yetu na tukumbuke namna na jinsi alivyotusaidia katika mambo mengine kumbuka matendo yake ya kale na hii itamuimarisha kila mmoja wetu kujua kuwa Mungu yule yule asiyebadilika aliyewasaidia baba zetu katika vita zao atajitokeza tena kwa namna nyingine kutusaidia

Zaburi 77:11-14 “Nitayakumbuka matendo ya Bwana; Naam, nitayakumbuka maajabu yako ya kale. Pia nitaitafakari kazi yako yote; Nitaziwaza habari za matendo yako. Ee Mungu, njia yako i katika utakatifu; Ni nani aliye mungu mkuu kama Mungu? Wewe ndiwe Mungu ufanyaye maajabu; Uliudhihirisha uweza wako kati ya mataifa.”

Ee Bwana usimuache msomaji wangu, na msikilizaji wangu na kila mtu duniani anayekutegemea wewe, usimwache akazimia moyo wakati wa taabu yake lakini umpe moyo wa ujasiri kama Daudi na nutupe ushindi katika vita zetu za maisha katika jina la Yesu Kristo amen!

Na. Rev Innocent Samuel Kamote.

Mkuu wa wajenzi mwenye Hekima!