Zaburi 109:1-3. “Ee Mungu wa sifa zangu,
usinyamaze, Kwa maana wamenifumbulia kinywa; Kinywa cha mtu asiye haki, cha
hila, Wamesema nami kwa ulimi wa uongo.
Naam, Kwa maneno ya chuki wamenizunguka, Wamepigana nami bure.”
Utangulizi:
Wote tutakuwa tunafahamu nguvu
kubwa iliyoko katika maneno, maneno yana nguvu!, yana nguvu kubwa kiasi cha
kuweza kujenga, yana nguvu kubwa kiasi cha kuweza kubomoa, yana uwezo wa
kuponya, yana uwezo wa kujeruhi, yana uwezo wa kutia moyo, yana uwezo wa
kuvunja moyo, Neno la Mungu linasema kuwa maneno yana uwezo wa kuleta mauti au
kuleta uzima unaona!
Mithali 18:20-21 “Tumbo la mtu litajazwa
matunda ya kinywa chake; Atashiba mazao ya midomo yake. Mauti na uzima huwa
katika uwezo wa ulimi; Na wao waupendao watakula matunda yake.”
Leo nataka tuzungumzie kile
ambacho Roho Mtakatifu anataka nikizungumzie kwaajili ya watu wake anaotaka
kuwasaidia na hii ni kuishi zaidi ya maneno hasi, Ujumbe huu ulinijia kwa lugha
ya kiingereza “Beyond the negative words”
lakini mimi nahudumia watu wanaozungumza Kiswahili, kwa hiyo nimeUita ujumbe
huu Kuishi zaidi ya maneno!, Kila
mtu aliyemwamini Mungu anapaswa kuishi zaidi ya maneno, hususani maneno hasi
yaani yale yanayokuja kwetu kupitia Shetani na mawakala wake ambao wanatutupia
maneno ili tuishi kwa mipaka, ili tukate tamaa, ili tuvunjike moyo, ili
tushindwe, ili tuogope, ili tusiendelee, ili tutawalike, ili kutuonea na
kutujeruhi, ili kuondoa ujasiri wetu, ili ususie na kadhalika, Roho Mtakatifu
amenituma nikutie moyo kwamba unaweza kuishi zaidi ya maneno, na kuwa wako
watakatifu waliotutangulia ambao kimsingi walishi zaidi ya maneno na wakapata
ushindi na kusonga mbele katika maisha yao ya kawaida na ya kiroho Ishi zaidi ya maneno, Tutajifunza somo
hili kuishi zaidi ya maneno kwa kuzingatia vipengele vitatu vifuatavyo:-
·
Maneno ya
kuvunja moyo.
·
Wanadamu
na maneno ya kuvunja moyo.
·
Kuishi
zaidi ya maneno
Maneno ya kuvunja moyo.
Mojawapo ya namna na jinsi Shetani
anavyowashambulia watu wa Mungu ni pamoja na kuwashambulia kwa maneno, hususani
maneno ya kuvunja moyo, Shetani anaweza kuwatumia watu yaani mawakala wake, na
wanaweza kuwa na sura yoyote ile, wanaweza kuwa ni waamini wenzako, waimbaji
wenzako katika kwaya, watumishi wenzako, wakristo wenzako ndugu au watu wa
karibu na wakati mwingine watu wa ulimwengu huu watakurushia maneno ya
kukuvunja moyo, ili ujihoji kama unastahili, uwe na mashaka, uwe na wasiwasi
hata kuhusu ahadi za Mungu, watakuhukumu, watakujaza woga na hofu,
watashambulia imani yako, watakuvunja moyo, wataiba furaha yako. Shetani anaweza
kutumia marafiki, maadui na jamii na wakati mwingine hata moyoni mwako unaweza
ukajihukumu! Kwamba labda wewe sio bora sana, wewe sio mwema sana, labda wewe
huwezi kufanikiwa, hutoboi, au Mungu amekuacha, maneno haya yatakushambulia
kama mshale yakitafuta kukuvunja moyo na kukukatisha tamaa na unaweza hata
kudhani kuwa labda wokovu kwako hauna maana au Mungu hana msaada kwako, Kristo
Yesu alishambuliwa kwa maneno wakati akiwa msalabani katika hali ya mateso.
Luka 23:35-37 “Watu wakasimama wakitazama.
Wale wakuu nao walikuwa wakimfanyia mzaha, wakisema, Aliokoa wengine; na
ajiokoe mwenyewe, kama ndiye Kristo wa Mungu, mteule wake. Wale askari nao
wakamfanyia dhihaka, wakimwendea na kumletea siki, huku wakisema, Kama wewe
ndiwe mfalme wa Wayahudi, ujiokoe mwenyewe.”
Luka 23:38-39 “Na juu yake palikuwa na
anwani; HUYU NDIYE MFALME WA WAYAHUDI. Na mmoja wa wale wahalifu waliotungikwa
alimtukana, akisema, Je! Wewe si Kristo? Jiokoe nafsi yako na sisi.”
Mathayo 27:39-43 “Nao waliokuwa wakipita
njiani wakamtukana, wakitikisa-tikisa vichwa vyao, wakisema, Ewe mwenye
kulivunja hekalu na kulijenga kwa siku tatu, jiokoe nafsi yako; ukiwa ndiwe
Mwana wa Mungu, shuka msalabani. Kadhalika na wale wakuu wa makuhani
wakamdhihaki pamoja na waandishi na wazee, wakisema, Aliokoa wengine, hawezi
kujiokoa mwenyewe. Yeye ni mfalme wa Israeli; na ashuke sasa msalabani, nasi
tutamwamini. Amemtegemea Mungu; na amwokoe sasa, kama anamtaka; kwa maana
alisema, Mimi ni Mwana wa Mungu.”
Neno la Mungu linaonya na
kukemea, likitaka wanadamu wawe na matumizi mazuri ya ulimi yaani maneno kwani
yanaweza kusababisha madhara makubwa sana, uharibifu wa aina nyingi sana
duniani na hata vita kubwa duniani zilianza na ulimi tu, talaka, majungu
makazini, kufukuzwa watu kazi, kuharibia wengine maisha kumesababishwa kwa
kiwango kikubwa na ulimi, yaani maneno maneno yameumiza wengi, yameua wengi,
yamefarakanisha wengi, yamechongea wengi na kuleta uharibifu katika maisha ya
wengi kiroho, kiakili, kiuchumi, kisaikolojia na kadhalika.
Yakobo 3:5-6 “Vivyo hivyo ulimi nao ni
kiungo kidogo, nao hujivuna majivuno makuu. Angalieni jinsi moto mdogo
uwashavyo msitu mkubwa sana. Nao ulimi ni moto; ule ulimwengu wa uovu, ule
ulimi, umewekwa katika viungo vyetu, nao ndio uutiao mwili wote unajisi,
huuwasha moto mfulizo wa maumbile, nao huwashwa moto na jehanum.”
Wanadamu na maneno ya kuvunja moyo
Hebu tuwe wakweli tu maneno ya
kuvunja moyo ni sehemu ya maisha ya Mwanadamu, tunaishi katika ulimwengu
uliooza na kuharibikwa kwa dhambi, kwa sababu hiyo aidha watu kwa kupenda au
hata kwa kutokupenda, kwa kudhamiria au hata kwa kutokudhamiria, watapiga domo,
watapiga umbeya, wanadamu ni wambeya wanadamu ni waongo wanadamu wana maneno
yaliyojaa sumu, wanadamu wana maneno, wanadamu ni wazushi, watu wana maneno
watu wanazungumza bhana maneno ya kuumiza, maneno ya kubomoa, maneno ya
kukosesha watu wanasengenya, ukiwa mwema utasengenywa, ukiwa mbaya
utasengenywa, vyovyote uwavyo kila mwanadamu anasemwa mahali fulani na wakati
mwingine wanazungumza maneno yanayoumiza sana, wanazungumza maneno ya kuharibu,
wanazungumza vitu vya kuharibu usalama wako, wanakuweka uchi, wanakuwekea
mipaka, wanaharibu maisha, na wakati mwingine wanatumiwa wazi wazi na adui Shetani
kuumiza na kukatisha tamaa wengine na hata waliookoka huingia katika mtego huu
na hata sisi wenyewe tunaweza kujifikiri vibaya kama hatutaacha kujitazama
katika mtazamo wa Mungu, kwa ujumla ndimi za wanadamu zimejaa sumu, yaani watu
wana maneno yenye madhara na wanaweza kuzungumza bila kujifikiri, hawafikiri
madhara, hawafikiri mauti wanatumiwa tu na yule shetani, ukitenda mema
watasema, ukitenda mabaya watasema ni mawakala wa Shetani.
Zaburi 140:1-3. “Ee Bwana, uniokoe na mtu
mbaya, Unihifadhi na mtu wa jeuri. Waliowaza mabaya mioyoni mwao, Kila siku
huondokesha vita. Wamenoa ndimi zao kama nyoka, Sumu ya fira i chini ya midomo
yao.”
Kwa hiyo utakubaliana nami kuwa
maneno ya kukatisha tamaa ni sehemu ya maisha ya kila siku na ya kawaida katika
ulimwengu huu wa watu wasio wakamilifu, Mwandishi wa Zaburi amewahi kulalamika
kuwa wakati mwingine hata rafiki zetu wa karibu wanaweza kutunenea mabaya, watu
tunaosali nao pamoja, marafiki na hata ndugu, yaani yeyote anaweza kutumiwa! Haijalishi
ni nani!
Zaburi 55:12-14 “Kwa maana aliyetukana si
adui; Kama ndivyo, ningevumilia. Aliyejitukuza juu yangu siye anichukiaye; Kama
ndivyo, ningejificha asinione. Bali ni wewe, mtu mwenzangu, Rafiki yangu,
niliyejuana nawe sana. Tulipeana shauri tamu; na kutembea Nyumbani mwa Mungu
pamoja na mkutano.”
Warumi 3:10-14 “kama ilivyoandikwa, ya
kwamba, Hakuna mwenye haki hata mmoja. Hakuna afahamuye; Hakuna amtafutaye
Mungu. Wote wamepotoka, wameoza wote pia; Hakuna mtenda mema, la! Hata mmoja.
Koo lao ni kaburi wazi, Kwa ndimi zao wametumia hila. Sumu ya fira i chini ya
midomo yao.Vinywa vyao vimejaa laana na uchungu.”
Endapo hutajifunza na kuelewa kwa
kina na mapana na marefu Neno la Mungu unaweza kusumbuka sana, lakini ukielewa
kuwa tuko Duniani na Dunia imejaa wazushi na waongo na waharibifu na wasema
vibaya na waumizaji hutaweza kuishi zaidi ya maneno “Beyond the negative words” Lakini ashukuriwe Mungu atupaye
kushinda Roho Mtakatifu atatuwezesha kuishi zaidi ya maneno, Maneno ni aina ya
vita, ambayo Shetani anaitumia, kama ilivyo katika ulimwengu wa kawaida
mabondia na wapiganaji kabla ya kupigana huanza na tambo za maneno au propaganda
hii ni vita ambayo watakatifu waliotutangulia waliifahamu na kujua namna na
jinsi ya kuipigana, kwa nini Shetani hutumia vita vya maneno kuwashambulia watu
wa Mungu hii ni kwa sababu:-
-
Unashambuliwa
ili ujisahau kuwa wewe ni nani – anataka usahahu kuwa wewe ni chagua la
Mungu na Mungu amekuumba kwa jinsi ya ajabu, amekuumba kwa kusudi na kwa
ushindi na kukuita kwenye kusudi lake kwa sababu hiyo ni lazima Shetani akushambulie,
akushitaki.
Zaburi 139:13-14 “Maana Wewe ndiwe uliyeniumba mtima wangu,
Uliniunga tumboni mwa mama yangu, Nitakushukuru kwa kuwa nimeumbwa Kwa jinsi ya
ajabu ya kutisha. Matendo yako ni ya ajabu, Na nafsi yangu yajua sana,”
1Petro 2:9-10 “Bali
ninyi ni mzao mteule, ukuhani wa kifalme, taifa takatifu, watu wa milki ya
Mungu, mpate kuzitangaza fadhili zake yeye aliyewaita mtoke gizani mkaingie
katika nuru yake ya ajabu; ninyi mliokuwa kwanza si taifa, bali sasa ni taifa
la Mungu; mliokuwa hamkupata rehema, bali sasa mmepata rehema.”
-
Unashambuliwa
ili utoke katika kusudi la Mungu – Maneno yanaweza kukutia mashaka na
kukufadhaisha ili ikiwezekana yakutoe katika mpango na mapenzi ya Mungu au kusudi
ambalo kwalo Mungu amekuitia
Nehemia 4:1-3 “Lakini
ikawa, Sanbalati aliposikia ya kwamba tulikuwa tukiujenga ukuta, akaghadhibika,
akaingiwa na uchungu sana, akawadhihaki Wayahudi. Akanena mbele ya nduguze na
mbele ya jeshi la Samaria, akisema, Wayahudi hawa wanyonge wanafanyaje? Je!
Watajifanyizia boma? Watatoa dhabihu? Au watamaliza katika siku moja? Je!
Watayafufua mawe katika chungu hizi za kifusi, nayo yameteketezwa kwa moto?
Basi Tobia, Mwamoni, alikuwa karibu naye, akasema, Hata hiki wanachokijenga,
angepanda mbweha, angeubomoa ukuta wao wa mawe.”
-
Unashambuliwa
kwaajili ya kuidhoofisha Imani – Maneno yanaweza kutumika kama njia ya
kukuvunja moyo, ili ushindwe kulitimiza kusudi la Mungu kwa Imani na kurudi
katika mashaka Israel walipokuwa wanakaribia kuingia katika inchi ya Kanaani
wapelelezi kumi walitumiwa na shetani wakwavunja moyo watu kwa maneno yao na
watu wakakubali kuvunjika moyo.
Hesabu 13:31-33 “Bali wale watu waliopanda pamoja naye
wakasema, Hatuwezi kupanda tupigane na watu hawa; kwa maana wana nguvu kuliko
sisi. Wakawaletea wana wa Israeli habari mbaya ya ile nchi waliyoipeleleza,
wakasema, Ile nchi tuliyopita kati yake ili kuipeleleza, ni nchi inayowala watu
wanaoikaa; na watu wote tuliowaona ndani yake ni watu warefu mno. Kisha, huko
tuliwaona Wanefili, wana wa Anaki, waliotoka kwa hao Wanefili; tukajiona nafsi
zetu kuwa kama mapanzi; nao ndivyo walivyotuona sisi.”
Hesabu 14:1-3 “Mkutano
wote wakapaza sauti zao wakalia; watu wakatoka machozi usiku ule. Kisha wana wa
Israeli wote wakamnung'unikia Musa na Haruni; mkutano wote wakawaambia,
Ingekuwa heri kama tungalikufa katika nchi ya Misri, au, ingekuwa heri kama
tungalikufa katika jangwa hili. Mbona Bwana anatuleta mpaka nchi hii ili
tuanguke kwa upanga? Wake zetu na watoto wetu watakuwa mateka; je! Si afadhali
turudi Misri?”
Kuishi zaidi ya maneno;
Ili kila mtu duniani awe na amani
ya kweli na ushindi dhidi ya maneno ya kukatisha tamaa na kuumiza moyo
tunayokuta nayo duniani basi inatulazimu kuishi zaidi ya maneno hasi, na ili
uweze kuishi zaidi ya maneno unapaswa kuishi kwa kuliangalia Neno la Mungu
linasema nini juu yako na sio kile watu wanachokisema, wewe na mimi sio matokeo
ya kile watu wanasema wewe na mimi ni matokeo ya kile Mungu anachokisema Neno
la Mungu lina nguvu kuliko nyundo ivunjayo mawe vipande vipande, Neno la Mungu
ni moto mkali wenye nguvu ya kuumba!
Yeremia 23:28-29 “Nabii aliye na ndoto, na
aseme ndoto yake; na yeye aliye na neno langu, na aseme neno langu kwa
uaminifu. Makapi ni kitu gani kuliko ngano? Asema Bwana. Je! Neno langu si kama
moto? Asema Bwana; na kama nyundo ivunjayo mawe vipande vipande?”
Watakatifu waliopata ushindi
katika kila vita waliyokutana nayo ya maneno walijikita katika Neno la Mungu na
ujuzi wao kuhusu Mungu, ukawafanya wawe washindi, wale walioogopa maneno
walinywea lakini wale walioliangalia neno la Mungu na kile Mungu ameahidi
hawakuogopa
a.
Daudi
na Gloiath – Walipigana vita vya maneno kwanza kabla ya kuingia katika vita
halisi, Goliathi aliogopewa sana sio tu kwa sababu ya ukubwa wake lakini pia
kwa sababu ya maneno yake hasi ambayo yalitisha sana na watu wote wakaogopa na
pia walimkimbia ilikuwa ni aibu kubwa sana. Lakini Daudi alifahamu namna ya
kushughulika naye. Daudi alikutana na maneno mengi ya kukatisha tamaa lakini
yeye aliishi zaidi ya maneno! Ona:-
1Samuel 17: 1-11 “Wakati
huo Wafilisti walikusanya majeshi yao kwa vita, nao wakakusanyika huko Soko,
ulio mji wa Yuda, wakatua kati ya Soko na Azeka, katika Efes-damimu. Naye Sauli
na watu wa Israeli wakakusanyika, wakatua katika bonde la Ela, nao wakapanga
vita juu ya hao Wafilisti.Wafilisti wakasimama juu ya mlima upande huu, na
Waisraeli wakasimama juu ya mlima upande huu, napo palikuwa na hilo bonde
katikati. Ndipo akatoka shujaa katika kambi ya Wafilisti, aliyeitwa Goliathi,
wa Gathi, ambaye urefu wake ulikuwa mikono sita na shibiri moja. Alikuwa na
chapeo ya shaba kichwani, tena amevaa darii ya shaba; na uzani wake ile darii
ya shaba ulikuwa shekeli elfu tano za shaba. Tena amevaa mabamba ya shaba
miguuni mwake, naye alikuwa na mkuki wa shaba kati ya mabega; yake. Na mti wa
fumo lake ulikuwa kama mti wa mfumaji; na kichwa cha mkuki wake kilikuwa
shekeli mia sita za chuma uzito wake; na mtu aliyemchukulia ngao yake
akamtangulia. Naye akasimama, akawapigia kelele majeshi ya Israeli akawaambia,
Mbona mmetoka kupanga vita? Je! Mimi si Mfilisti, na ninyi si watumishi wa
Sauli? Jichagulieni mtu, akanishukie mimi. Kama akiweza kupigana nami na
kuniua, sisi tutakuwa watumwa wenu; nami nikimshinda yeye na kumwua, ninyi
mtakuwa watumwa wetu, na kututumikia. Yule Mfilisti akasema, Nayatukana leo
majeshi ya Israeli; nipeni mtu tupigane. Basi Sauli na Israeli wote waliposikia
maneno hayo ya Mfilisti, wakafadhaika na kuogopa sana.”
1Samuel 17:24-28 “Na
watu wote wa Israeli walipomwona yule mtu wakakimbia, wakaogopa sana. Watu wa
Israeli wakasema, Je! Mmemwona mtu huyu aliyepanda huko? Hakika ametokea ili
awatukane Israeli; basi, itakuwa, mtu yule atakayemwua, mfalme atamtajirisha
kwa utajiri mwingi, naye atamwoza binti yake, na kuifanya mbari ya baba yake
kuwa huru katika Israeli. Daudi akaongea na watu waliosimama karibu, akisema,
Je! Atafanyiwaje yeye atakayemwua Mfilisti huyo, na kuwaondolea Israeli aibu
hii? Maana Mfilisti huyu asiyetahiriwa ni nani hata awatukane majeshi ya Mungu
aliye hai? Nao watu wakamjibu vivyo hivyo, wakisema, Ndivyo atakavyofanyiwa mtu
yule atakayemwua. Naye Eliabu, mkubwa wake, alisikia hapo alipoongea na watu;
na hasira yake Eliabu ikawaka juu ya Daudi, akasema, Mbona wewe umeshuka hapa?
Na kondoo wale wachache umemwachia nani kule nyikani? Mimi nakujua kiburi
chako, na ubaya wa moyo wako; maana umeshuka ili upate kuvitazama vita.”
1Samuel 17:32-33 “Daudi
akamwambia Sauli, Asizimie moyo mtu ye yote kwa ajili ya huyu; mimi mtumishi
wako nitakwenda kupigana na Mfilisti huyu. Sauli akamwambia Daudi, Huwezi wewe
kumwendea Mfilisti huyu upigane naye; maana wewe u kijana tu; na huyu ni mtu wa
vita tangu ujana wake.”
1Samuel 17:37 “Daudi
akasema, Bwana aliyeniokoa na makucha ya simba, na makucha ya dubu, ataniokoa
na mkono wa Mfilisti huyu. Sauli akamwambia Daudi, Enenda, na Bwana atakuwa
pamoja nawe.”
1Samuel 17:42-46 “Hata Mfilisti alipotazama huku na huku,
akamwona Daudi akamdharau; kwa kuwa ni kijana tu mwekundu, tena ana sura nzuri.
Mfilisti akamwambia Daudi, Je! Mimi ni mbwa hata umenijia kwa fimbo? Mfilisti
akamlaani Daudi kwa miungu yake. Mfilisti akamwambia Daudi, Njoo huku kwangu;
nyama yako nitawapa ndege wa angani na wanyama wa mwituni. Ndipo Daudi
akamwambia yule Mfilisti, Wewe unanijia mimi na upanga, na fumo, na mkuki, bali
mimi ninakujia wewe kwa jina la Bwana wa majeshi, Mungu wa majeshi ya Israeli
uliowatukana.Siku hii ya leo Bwana atakuua mkononi mwangu, nami nitakupiga, na
kukuondolea kichwa chako, nami leo nitawapa ndege wa angani na wanyama wa nchi
mizoga ya majeshi ya Wafilisti, ili kwamba dunia nzima wajue ya kuwa yuko Mungu
katika Israeli.”
Daudi ni mfano
wa watu ambao hawakukubali kuishi kwa maneno ya kukatisha tamaa kama
angeyasikiliza aibu kubwa ingelipata taifa zima la Israel, lakini aliishi zaidi
ya maneno alimkiri Mungu mwenye nguvu aliyeweza kumuokoa yeye na wanyama wakali
wakiwepo simba na dubu akitambua ya kuwa Mungu huyu na neno lake ana nguvu
kuliko maneno na umbile la adui
b.
Hanna
na Penina – Hana alipata maneno ya kuumiza na kukatisha tamaa kutoka kwa
Penina kwa sababu Hana hakuwa na watoto, alichokozwa na kusemwa vibaya kwa
maneno hasi Penina alifanya hivyo mwaka kwa mwaka mpaka Hana aliacha kula na
kusikitishwa sana naye
1Samuel 1:6-7 “Ila
mwenzake humchokoza sana, hata kumsikitisha, kwa sababu Bwana alikuwa amemfunga
tumbo. Tena mumewe akafanya hivyo mwaka kwa mwaka, hapo yule mwanamke alipokwea
kwenda nyumbani kwa Bwana, ndivyo yule alivyomchokoza; basi, kwa hiyo, yeye
akalia, asile chakula.”
Hata pamoja na
maneno ya kuumiza na kukatisha tamaa Hana alifamya uamuzi wa kuishi zaidi ya
maneno yeye aliongeza kasi kwenye maombi na kumlilia Mungu na Mungu
hakumuangusha kwani alimjibu na kumpa mtoto Samuel na watoto wengine, kinywa
cha Hana kilizungumza lugha nyingine kwa furaha
1Samuel 2:1-10 “Naye
Hana akaomba, akasema, Moyo wangu wamshangilia Bwana, Pembe yangu imetukuka
katika Bwana, Kinywa changu kimepanuka juu ya adui zangu; Kwa kuwa naufurahia
wokovu wako; Hakuna aliye mtakatifu kama Bwana; Kwa maana hakuna ye yote ila
wewe, Wala hakuna mwamba kama Mungu wetu. Msizidi kunena kwa kutakabari hivyo;
Majivuno yasitoke vinywani mwenu; Kwa kuwa Bwana ni Mungu wa maarifa, Na
matendo hupimwa na yeye kwa mizani. Pinde zao mashujaa zimevunjika, Na hao
waliojikwaa wamefungiwa nguvu. Walioshiba wamejikodisha ili kupata chakula, Na
hao waliokuwa na njaa wamepata raha. Naam, huyo aliyekua tasa amezaa watoto
saba, Na yeye aliye na wana wengi amedhoofika. Bwana huua, naye hufanya kuwa
hai; Hushusha hata kuzimu, tena huleta juu. Bwana hufukarisha mtu, naye
hutajirisha; Hushusha chini, tena huinua juu. Humwinua mnyonge kutoka
mavumbini, Humpandisha mhitaji kutoka jaani, Ili awaketishe pamoja na wakuu,
Wakakirithi kiti cha enzi cha utukufu; Kwa maana nguzo za dunia zina Bwana,
Naye ameuweka ulimwengu juu yake. Yeye atailinda miguu ya watakatifu wake; Bali
waovu watanyamazishwa gizani, Maana kwa nguvu hakuna atakayeshinda; Washindanao
na Bwana watapondwa kabisa; Toka mbinguni yeye atawapigia radi; Bwana ataihukumu
miisho ya dunia; Naye atampa mfalme wake nguvu, Na kuitukuza pembe ya masihi
wake.”
Kaka zangu na
dada zangu Mungu anatutaka tuishi zaidi maneno, hatuishi kwa sababu ya maneno
ya watu tunaishi kwa sababu ya neno la Mungu, ushindi wa maisha yetu umefungwa
katika neno la Mungu na sio katika maneno ya wanadamu sisi ni washindi na zaidi
ya kushinda. Hakikisha katika maisha yako unajaa neno la Mungu ili kila neno
utakaloshambuliwa uwe unajibu lake katika neno la Mungu Ni neno la Mungu tu litakaloulinda
moyo wako na mashambulizi ya shetani, litaiweka sawa akili yako litakulinda na
kukuhifadhi maneno ya kukatisha tamaa
hayatakuwa na nguvu kwa mtu aliyejaa neno la Mungu ushindi wako utakuwa kama
Daudi dhidi ya Goliati na Hana dhidi ya Penina, au Nehemia na akina Sanbalati,
jifiche katika neno la Mungu imba ahadi zake kumbuka hakuna silaha
itakayofanyika juu yako ambayo itafanikiwa na kila ulimi utakaoinuka dhidi yako
katika kuhukumu utauhukumu kuwa mkosa na huu ndio urithi wa watumishi wa Mungu!
Isaya 54:17 “Utathibitika
katika haki; utakuwa mbali na kuonewa, kwa maana hutaogopa; na mbali na hofu,
kwa maana haitakukaribia.Tazama, yamkini watakusanyana; lakini si kwa shauri
langu. Watu wo wote watakaokusanyana juu yako wataanguka kwa ajili yako. Tazama,
nimemwumba mhunzi avukutaye moto wa makaa, akatoa silaha kwa kazi yake; nami nimemwumba
mharibu ili aharibu. Kila silaha itakayofanyika juu yako haitafanikiwa na kila
ulimi utakaoinuka juu yako katika hukumu utauhukumu kuwa mkosa. Huu ndio urithi
wa watumishi wa Bwana, na haki yao inayotoka kwangu mimi, asema Bwana.”
Na Rev. Innocent Samuel Kamote