Jumapili, 16 Novemba 2025

Msigombane njiani!


Mwanzo 45:21-24 “Ndivyo walivyofanya wana wa Israeli. Yusufu akawapa magari kama Farao alivyoamuru, akawapa na chakula cha njiani. Akawapa kila mtu nguo za kubadili; lakini Benyamini, alimpa fedha mia tatu na mavazi matano ya kubadili. Na babaye akampelekea kama hivi, punda kumi waliochukua mema ya Misri, na punda wake kumi waliochukua nafaka, na mikate, na chakula kwa babaye njiani. Akaagana na ndugu zake, wakaenda zao; naye akawaambia, Msigombane njiani.




Utangulizi:

Mojawapo ya agizo la msingi na la muhimu sana lililotolewa na Yusufu kwa ndugu zake ni pamoja na agizo hili, la “Msigombane njiani”, Agizo hili lilikuwa ni la muhimu na lenye kujenga umoja na amani ya kitaifa na kifamilia, hasa baada ya mafarakano, toba na msamaha na mapatano baada ya wana wa Israel kumuuza ndugu yao Yusufu utumwani ambako kwa neema ya Mungu alipata madaraka makubwa na akajitambulisha kwao, Yusufu anatoa maagizo haya ili kuilinda jamii yake wasiwe na mafarakano katika wakati wa mpito, kuelekea kwenye kuishi pamoja kwa furaha na amani kupitia mwaliko wake kwa familia nzima waje kuishi katika inchi ya Misri, wana wa Israel wangeliweza kuanza kushutumiana na kulaumiana kwaajili ya mambo yaliyopita wakati Yusufu amekwisha kutoa msamaha, maneno ya Yusufu kwao yanasimama kama onyo lenye kuweka msingi wa kuepusha migogoro njiani.

Neno la Mungu linaonya vikali kwamba katika vitu ambavyo ni chukizo kubwa kwa Mungu ni pamoja na kupanda mbegu ya fitina kati ya ndugu, yaani kugombanisha watu, Yusufu hakutaka kutoa ruhusa kwa ndugu zake ambao kimsingi aliwapima na kujua kuwa wamebadilika sana mioyoni mwao kwa hiyo asingelitoa nafasi ya wao kufarakana na kuumizana kwa sababu ya fitina na ugomvi kama wa mwanzo uliowafarakanisha wao na yeye kwa ndugu zake.

Mithali 6:16-19 “Kuna vitu sita anavyovichukia Bwana; Naam, viko saba vilivyo chukizo kwake. Macho ya kiburi, ulimi wa uongo, Na mikono imwagayo damu isiyo na hatia;Moyo uwazao mawazo mabaya; Miguu iliyo myepesi kukimbilia maovu; Shahidi wa uongo asemaye uongo; Naye apandaye mbegu za fitina kati ya ndugu.”

Yusufu alikuwa amefahamu mpango wa Mungu, kwamba watu wanaweza kufarakana na kufitiniana lakini Mungu akawa amekusudia jambo jema katika fitina hizo na kutimiza mpango wake, kwa sababu hiyo sasa ulikuwa ni wakati wa kuhakikisha kuwa familia inakuwa na umoja, na inalinda mpango wa Mungu wa kuwa na amani, na kwa sababu hiyo agizo lake sio adhabu, bali ni somo la kiroho kwa jamii yake, taifa lake na ndugu zake kwamba wasigombane tena kwa sababu Mungu amekwisha kutimiza mpango wake kwao! Tutajifunza somo hili Msigombane njiani kwa kuzingatia vipengele muhimu vitatu vifuatavyo:-

·         Maana ya kugombana njiani

·         Msigombane njiani

·         Athari za kugombana njiani


Maana ya kugombana njiani

Mwanzo 45:21-24 “Ndivyo walivyofanya wana wa Israeli. Yusufu akawapa magari kama Farao alivyoamuru, akawapa na chakula cha njiani. Akawapa kila mtu nguo za kubadili; lakini Benyamini, alimpa fedha mia tatu na mavazi matano ya kubadili. Na babaye akampelekea kama hivi, punda kumi waliochukua mema ya Misri, na punda wake kumi waliochukua nafaka, na mikate, na chakula kwa babaye njiani. Akaagana na ndugu zake, wakaenda zao; naye akawaambia, Msigombane njiani.

Moja ya jambo ambalo linavuruga sana umoja wa kifamilia, kitaifa na kijamii ni pamoja na ugomvi, kugombana kuna athari kubwa sana yaani athari hasi katika maisha ya mtu mmoja mmoja, wanandoa, jamii na taifa, watu wanaogombana wanaharibiana na kuleteana athari kubwa sana kimaisha, kihisia na mahusiano na kuacha majeraha ya uchungu, hasira, kisasi, chuki na mgawanyiko, kwa ujumla ninaweza kusema hakuna sumu mbaya katika mahusiano kama ugomvi, watu wanapoanza kugombana, kuchukiana na kuchochea hasira na migawanyiko, mwelekeo wake unakuwa ni kutengeneza matatizo makubwa zaidi yanayoharibu maisha hususani ya wale wanaohusika katika ugomvi huo, akilijua hili Yusufu katika hekima yake na akili yake aliwaonya ndugu zake kuwa wasigombane njiani!, kama kuna jambo huwa linasikitisha sana katika jamii ni kuishi katika jamii inayogombana!

Kugombana njiani hasa maana yake ni nini? Katika lugha ya asili ya Kiebrania neno kugombana linasomeka kama neno “ragaz” au “tirgәzῡ” kwa Kiyunani “orgizethe”, au “orgē” maana zake kwa kiingereza ni  fall not out”, “quarrel”, “argue”, “become troubled”, “disagree in words”, kwa Kiswahili tunaweza kusema “Msikosoane”, au “msikoseane”, “Msigombane” au “msibishane”, Msisumbuane”, au msileteane taabu, msisumbuane kwa meneno, au msikose kufikia muafaka,  na neno njia kwa kiyunani ni “hodō” ambalo maana yake ni safari ya maisha, kwa hiyo sio tu njia ya kawaida lakini katika maisha, kwa msingi huo neno la Mungu linamtaka kila mmoja katika jamii, wanandoa, kanisa, ndugu, jamaa, marafiki na taifa lolote kwamba wasigombane njiani, yaani wasiwe na mafarakano katika safari ya maisha, watu waache kuwa na uchungu, waache hasira, wasiwe watu wasiofikia muafaka, kimsingi mafarakano yoyote humzimisha Roho Mtakatifu na kuondoa maarifa, hekima na busara katika mioyo ya watu.

Yusufu alikuwa na ufahamu kuwa mambo mabaya yanaweza kutokea pale watu, ndugu, wanandoa au jamii na taifa kwa ujumla wakiruhusu magomvi, wanafungua ufunguo wa shina la uchungu, kupoteza umoja, kuruhusu mafarakano, migawanyiko na hata mauaji lakini sio hivyo tu watu wanaogombana wanafanya upumbavu na kumuhuzunisha Roho Mtakatifu, na kuthibitisha kuwa wao bado hawana ukomavu wa kiroho, kiakili na kifikra na wanaharibu uhusiano wao na Mungu na kutengeneza kizuizi kwa maombi na baraka za Mungu zilizokusudiwa katika maisha yao. Ugomvi huwaweka watu katika vifungo vya kiroho na kuweka ukwazo wa wao kufunguliwa na kuwahuru

Mithali 20:3 “Mtu kujitenga na ugomvi ni heshima kwake; Bali kila mpumbavu ataka kugombana”.

Mathayo 5:22-26.“Bali mimi nawaambieni, Kila amwoneaye ndugu yake hasira itampasa hukumu; na mtu akimfyolea ndugu yake, itampasa baraza; na mtu akimwapiza, itampasa jehanum ya moto. Basi ukileta sadaka yako madhabahuni, na huku ukikumbuka ya kuwa ndugu yako ana neno juu yako, iache sadaka yako mbele ya madhabahu, uende zako, upatane kwanza na ndugu yako, kisha urudi uitoe sadaka yako. Patana na mshitaki wako upesi, wakati uwapo pamoja naye njiani; yule mshitaki asije akakupeleka kwa kadhi, na kadhi akakupeleka kwa askari, ukatupwa gerezani. Amin, nakuambia, Hutoki humo kamwe hata uishe kulipa senti ya mwisho.”

Msigombane njiani.

Mwanzo 45:24 “Akaagana na ndugu zake, wakaenda zao; naye akawaambia, Msigombane njiani.”  Kimsingi Yusufu alitoa agizo Msigombane njiani akiwa na uzoefu wa kutosha na mpana sana wa kutaka kuilinda jamii yake, kama kila Taifa, Kanisa, wanandoa  na jamii wanataka kujilinda ana aibu na kujilinda na kumpa shetani nafasi hawana budi kujilinda na mafarakakano, na ugomvi usio na tija, mtu mmoja Mwalimu wa zamani sana wa chuo cha Biblia Dodoma (AGBC) kwa sasa (CBC) Mwalimu Ndosi mwaka 2000 alisema hivi nanukuu “Watu wanapopendana huwa hatuulizi kwanini wamependana na wala hatuwaingilii, lakini watu wanapogombana tunaingilia na kuuliza ni kwanini wanagombana” mwisho wa kunukuu, Mwalimu Ndosi alikuwa anamaanisha kuwa watu wanapopendana huwa hakuna kelele kwa hiyo hakuna mtu anayesikia na kujua kuwa nini kinaendelea lakini watu wanapogombana kunakuwa na makelele na hivyo watu wengine huja kuingilia na kuuliza kwa nini mnagombana, ugomvi huleta aibu, na kumfanya kila mtu hata majirani kujiuliza kwanini hawa wanagombana, mnapopendana hakuna vikao, mnapogombana vikao vinaanza, mnapopendana mnafukuza maadui mnapogombana maadui wenu huanza kupata mwanya wa kuwaingilia na kuwavuruga zaidi hii ni kuanzia ngazi ya familia hadi ngazi ya kitaifa, hususani katika nyakati za leo ambako kuna uwazi mkubwa wa vyombo vya habari na mitandao ya kijamii hamuwezi kujificha, Kaini na Habili walipoanza kuwa na mzozo kwa sababu ya wivu wa Kaini kwa nduguye, Mungu aliingilia kati na kuanza kuuliza, lakini walipoishi kwa umoja, amani na upendo hata Mungu hakuuliza maswali, kwani hali ilikuwa shwari.

Mwanzo 4:3-11 “Ikawa hatimaye Kaini akaleta mazao ya ardhi, sadaka kwa BWANA. Habili naye akaleta wazao wa kwanza wa wanyama wake na sehemu zilizonona za wanyama. BWANA akamtakabali Habili na sadaka yake; bali Kaini hakumtakabali, wala sadaka yake. Kaini akaghadhibika sana, uso wake ukakunjamana. BWANA akamwambia Kaini, Kwa nini una ghadhabu? Na kwa nini uso wako umekunjamana? Kama ukitenda vyema, hutapata kibali? Usipotenda vyema dhambi iko, inakuotea mlangoni, nayo inakutamani wewe, walakini yapasa uishinde. Kaini akamwambia Habili nduguye, [Twende uwandani]Ikawa walipokuwapo uwandani, Kaini akamwinukia Habili nduguye,akamwua. BWANA akamwambia Kaini, Yuko wapi Habili ndugu yako? Akasema, Sijui, mimi ni mlinzi wa ndugu yangu? Akasema, Umefanya nini? Sauti ya damu ya ndugu yako inanililia kutoka katika ardhi. Basi sasa, umelaaniwa wewe katika ardhi, iliyofumbua kinywa chake ipokee damu ya ndugu yako kwa mkono wako;”

Kaini hakutenda haki, hakufanya vizuri, lakini Habili alitenda haki na alifanya vizuri, waliishi kwa utulivu lakini walipoanza kugombana Mungu alisikia ugomvi wao, Mungu aliingilia kati na Mungu alielekeza njia ya kufanya, Mungu amekusudia kumpa kibali kila mmoja, na amekusudi kumbariki kila mmoja jambo la msingi ni kila mtu kusimama katika wajibu wake na kutenda haki,  UKITENDA VEMA HUTAPATA KIBALI? agizo la kutokugombana njiani lilikuwa linamtaka kila mmoja kutokuwa sababu ya ugomvi na sababu ya malumbano katika jamii, kama viko vyama vya siasa vyama hivyo vina wajibu wa kuwatumikia wananchi na kuwatendea haki na kuwaletea maendeleo, tuko katika safari ya kuelekea kwenye kilele cha maendeleo na hakuna sababu ya kugombana njiani, kama mtu anahisi kupoteza kibali, njia sahihi ni kufanya vizuri na kutokugombana, kila mmoja anapaswa kutimiza wajibu kwa maslahi mapana ya jamii na sio kwa manufaa ya watu wachache na ubinafsi, Yusufu aliwaasa ndugu zake kutokugombana sio kwa maslahi yao tu bali na masalahi ya familia nzima, alitaka kumlinda na Yakobo Baba yake, alifahamu kuwa ugomvi wa ndugu hawa njiani pia ungemuathiri Baba yao, ambaye alikuwa amedanganywa kuwa Yusufu amekufa na wakachukua kanzu yake na kuichana chana na kuitia damu na kumwambia Baba yao kuwa Yusufu amekufa!, Ugomvi wao ungemuhuzunisha mzee kule nyumbani na hasa kama sasa angejua ukweli kuwa sasa Yusufu yuko hai!.

Mwanzo 37:31-34 “Wakaitwaa kanzu ya Yusufu, wakachinja mwana-mbuzi, na kuichovya kanzu katika damu. Wakaenda nayo ile kanzu ndefu, wakamletea baba yao, wakasema, Tumeona hii; basi, utambue kama kanzu hii ni ya mwanao, ama siyo. Akaitambua, akasema, Ndiyo kanzu ya mwanangu, mnyama mkali amemla; bila shaka Yusufu ameraruliwa. Yakobo akararua mavazi yake, akajivika gunia viunoni, na kumlilia mwanawe siku nyingi.”

Yusufu alikuwa anajua kuwa ugomvi wa kifamilia, kitaifa na kijamii unawahuzunisha sana wazee, alifahamu kuwa mgogoro wao unaweza kuwafikia wazazi na kuwafanya walie na kuhuzunika, wazee wetu ambao wametulea kwa shida na taabu mpaka tumekua wametuoza, wametusomesha na kuhakikisha ya kuwa tuna maisha haya tuliyo nayo wamestaafu na kutulia nyumbani, wamelitumikia taifa hili na kulipigania, wamepambana tangu kuipatia uhuru nchi yetu hatuwezi kuwalipa upumbavu, hatuwezi kuwapelekea maiti wala kanzu zilizojaa damu, mgogoro wa Kaini na Habili ulimuhuzunisha Adamu, migogoro yetu na ugomvi unahuzunisha watu wasio na hatia na kuwafanya wahuzunike na kujisikia vibaya, Mzozo na ugomvi ni aibu kubwa sana kwa familia, jamii na taifa msigombane njiani.

Wazee wetu wanahitaji habari njema, wanahitaji mavazi, chakula utulivu, Amani na kula mema ya nchi waliyoyataabikia na hawahitaji tena kusikia magomvi, wanahitaji kucheza na wajuu zao na sio kupelekewa kanzu zilizojaa damu, wala kupelekewa kazi ya kutatua migogoro ya ndoa zenu, wala kusikia habari mbaya wanahitaji habari njema iliyokamilika, mioyo yao ichangamke, Yakobo alipopokea habari njema roho yake ilifufuka ndani yake

Mwanzo 45:21-24 “Ndivyo walivyofanya wana wa Israeli. Yusufu akawapa magari kama Farao alivyoamuru, akawapa na chakula cha njiani. Akawapa kila mtu nguo za kubadili; lakini Benyamini, alimpa fedha mia tatu na mavazi matano ya kubadili. Na babaye akampelekea kama hivi, punda kumi waliochukua mema ya Misri, na punda wake kumi waliochukua nafaka, na mikate, na chakula kwa babaye njiani. Akaagana na ndugu zake, wakaenda zao; naye akawaambia, Msigombane njiani.

Mwanzo 45:26-28 “Wakampasha habari, wakisema, Yusufu angali hai; naye ndiye mtawala katika nchi yote ya Misri. Moyo wake ukazimia, kwa sababu hakuwasadiki. Wakamwambia maneno yote ya Yusufu, aliyowaambia; na alipoona magari aliyoyapeleka Yusufu, ili kumchukua, roho ya Yakobo baba yao ikafufuka.Israeli akasema, Yatosha! Yusufu mwanangu angali hai; nitakwenda, nionane naye kabla sijafa.”

Israel/Yakobo alipopewa habari njema roho yake ikafufuka alisema neno moja tu YATOSHA hakutaka kusikia habari nyingine alijawa na furaha, aliona na magari aliyoletewa na mwanae; Je ugomvi wetu una manufaa gani kwa jamii, unamanufaa gani kwa watoto wetu, una manufaa gani kwa wanawake una manufaa gani hata kwetu wenyewe, ROHO YAKE IKAFUFUKA katika Kiebrania linatumika neno “Châyâh” kwa kiingereza “recovered” au “repaired” Yakobo alipokea uponyaji wa roho yake kwa sababu alipokea habari njema na akasema “Yatosha” ameridhishwa na habari njema na taarifa njema hiki ndio familia inataka kusikia, hiki ndicho jamii inataka kusikia, hiki ndio taifa na watu wa Mungu yaani kanisa tunataka kusikia, habari za ugomvi na mafarakano katika jamii huongeza migandamizo ya mawazo, hurudisha watu nyuma, huleta majeraha na vidonda vya moyo na kuufisha moyo tuache kugombana!

Yusufu aliweka katazo lenye kuleta Baraka na kujenga umoja wa kijamii,kifamilia na kitaifa ambao kimsingi unaruhusu uwepo wa Mungu na kusababisha baraka kubwa sana, safari ya kutoka Misri mpaka Kanaani kwa kutembea pamoja na punda na ngamia ingeweza kuchukua kati ya siku 10 -14 muda huu kama usingelikuwa na onyo kama hili la msigombane njiani wangefika wakiwa wamevurugana vya kutosha lakini pia ilikuwa aibu kwa wageni waliombatana nao kwa magari maalumu yaliyokuwa yanaenda kumpelekea Yakobo zawadi na kumchukua kuja Misri

Zaburi 133:1-3 “Tazama, jinsi ilivyo vema, na kupendeza, Ndugu wakae pamoja, kwa umoja. Ni kama mafuta mazuri kichwani, Yashukayo ndevuni, ndevu za Haruni, Yashukayo mpaka upindo wa mavazi yake. Kama umande wa Hermoni ushukao milimani pa Sayuni. Maana ndiko Bwana alikoamuru baraka, Naam, uzima hata milele.”          

Athari za kugombana njiani.

Neno la Mungu linatupa uwanja mpana wa kuelewa kuwa ugomvi una athari hasi, na zenye kuharibu, mahusiano ya kijamii na maisha ya kiroho, watu wanaoanzisha magomvi wanafananishwa na watu au mtu anayetoboa mtumbwi ukiwa kwenye maji, na mafuriko yanaweza kuuzamisha na safari ikakwama.

Mithali 17:12-14 “Afadhali mtu akutwe na dubu aliyenyang'anywa watoto wake, Kuliko na mpumbavu katika upumbavu wake. Yeye arudishaye mabaya badala ya mema, Mabaya hayataondoka nyumbani mwake. Mwanzo wa ugomvi ni kama kutoboa penye maji; Basi acheni ugomvi kabla haujafurika.”

Kwa hiyo tunajifunza kwamba kuna madhara au athari kubwa sana ya kimwili na kiroho na hata kisaikolojia inayosababishwa na ugomvi, na huenda Yusufu mwana wa Yakobo alikuwa na ufahamu huo na alitaka kuilinda na kuitunza familia yake kiroho na kimwili ili wawe na uhusiano mzuri na Mungu na pia wawe na uhusiano mzuri wao kwa wao hapa ziko athari kadhaa zitokanazo na kugombana njiani:-

Ø  Kutokugombana njiani kunatujengea uhusiano mwema na Mungu, wakati migogoro na ugomvi unaweza kuharibu mawasiliano yetu na Mungu na kuzuia maombi na ibada, kutokugombana kuna athari chanya kwani kunatujengea uhusiano mwema na Mungu.  Wanandoa wanaogombana sio tu kuwa wanaiweka ndoa yao rehani, lakini pia wajue ibada zao, maombi yao na dua zao haziwezi kukubalika kwa Mungu kama kuna mtu hujamalizana naye, hujapatana naye na kuweka mambo vizuri, ibada yako na sadaka yako hazikubaliwi

 

1Petro 3:7-9 “Kadhalika ninyi waume, kaeni na wake zenu kwa akili; na kumpa mke heshima, kama chombo kisicho na nguvu; na kama warithi pamoja wa neema ya uzima, kusudi kuomba kwenu kusizuiliwe. Neno la mwisho ni hili; mwe na nia moja, wenye kuhurumiana, wenye kupendana kama ndugu, wasikitikivu, wanyenyekevu; watu wasiolipa baya kwa baya, au laumu kwa laumu; bali wenye kubariki; kwa sababu hayo ndiyo mliyoitiwa ili mrithi baraka.”

 

Mathayo 523-24 “Basi ukileta sadaka yako madhabahuni, na huku ukikumbuka ya kuwa ndugu yako ana neno juu yako, iache sadaka yako mbele ya madhabahu, uende zako, upatane kwanza na ndugu yako, kisha urudi uitoe sadaka yako.”

 

Ø  Ugomvi ni dalili ya kutokukomaa kiroho na kifikra – Paulo mtume anawaona watu wenye mafarakano kama watu waliokosa ukomavu, watu walio wachanga na wenye kuonyesha udunia kama ni Wakristo basi wanaitwa Wakristo wa mwilini. Lakini jamii yoyote ile isiyokuwa na ukomavu na subira hishia katika ugomvi

 

1Wakorintho 3:1-3 “Lakini, ndugu zangu, mimi sikuweza kusema nanyi kama na watu wenye tabia ya rohoni, bali kama na watu wenye tabia ya mwilini, kama na watoto wachanga katika Kristo. Naliwanywesha maziwa sikuwalisha chakula; kwa kuwa mlikuwa hamjakiweza. Naam, hata sasa hamkiwezi,kwa maana hata sasa ninyi ni watu wa tabia ya mwilini. Maana, ikiwa kwenu kuna husuda na fitina, je! Si watu wa tabia ya mwilini ninyi; tena mnaenenda kwa jinsi ya kibinadamu?

 

Ø  Ugomvi humuuzunisha Roho Mtakatifu – watu wa Mungu wanapojihusisha na ugomvi, hasira, ghadhabu, uchungu, kelele na matukano ambayo kimsingi ni matunda au matokeo ya ugomvi humuuzunisha Roho Mtakatifu na kuanza kumfifisha katika kanisa la Mungu na jamii na taifa.

 

Waefeso 4:29-31 “Neno lo lote lililo ovu lisitoke vinywani mwenu, bali lililo jema la kumfaa mwenye kuhitaji, ili liwape neema wanaosikia. Wala msimhuzunishe yule Roho Mtakatifu wa Mungu; ambaye kwa yeye mlitiwa muhuri hata siku ya ukombozi.Uchungu wote na ghadhabu na hasira na kelele na matukano yaondoke kwenu, pamoja na kila namna ya ubaya;”

               

Ø  Ugomvi unaweza kuwakosesha watu ufalme wa Mungu – Ugomvi ni moja ya matunda ya mwili au kazi za mwili, na wote wanaohusika na ugomvi kamwe hawawezi kuurithi ufalme wa Mungu.

 

Wagalatia 5:19-21 “Basi matendo ya mwili ni dhahiri, ndiyo haya, uasherati, uchafu, ufisadi, ibada ya sanamu, uchawi, uadui, ugomvi, wivu, hasira, fitina, faraka, uzushi, husuda, ulevi, ulafi, na mambo yanayofanana na hayo, katika hayo nawaambia mapema, kama nilivyokwisha kuwaambia, ya kwamba watu watendao mambo ya jinsi hiyo hawataurithi ufalme wa Mungu.”

 

Ø  Ugomvi ni hekima ya Shetani – Ugomvi ni chanzo na sababu ya dhambi nyingine, Shetani katika hekima yake anajua namna na jinsi ya kuondoa Amani miongoni mwa wanajamii na taifa kwa sababu hiyo ugomvi ni hekima ya shetani anajua kabisa katika magomvi atazalisha kiburi, mafarakano na kusababisha uharibifu mkubwa utakaozaa dhambi nyingine ikiwezekana hata mauaji, sio hivyo tu ataondoa Amani  kwa mfano hata wanandoa hawawezi kufurahia ndoa kama ugomvi unakuwa ni moja ya mtindo wa maisha kwa hiyo upendo huathiriwa, Yakobo anaonyesha kuwa hii ni hekima ya kishetani kwani yeye ndiye sababu ya machafuko!

 

Yakobo 3:15-17 “Hekima hiyo siyo ile ishukayo kutoka juu, bali ni ya dunia, ya tabia ya kibinadamu, na Shetani. Maana hapo palipo wivu na ugomvi ndipo palipo machafuko, na kila tendo baya. Lakini hekima itokayo juu, kwanza ni safi, tena ni ya amani, ya upole, tayari kusikiliza maneno ya watu, imejaa rehema na matunda mema, haina fitina, haina unafiki.”

Hitimisho:

Neno la Mungu linatuagiza kwamba tutafute kwa bidii kuwa na amani na watu wote, nyakati za Biblia wazee wetu walihakikisha kuwa wanatafuta Amani kwa bidii, kwa kuwa tuko duniani hitilafu zinaweza kutokea lakini hitimisho lililobora kwa watu wa Mungu na watu wenye busara ni kuhakikisha kuwa wanazika tofauti zao na kuitafuta Amani kwa bidii na huo ndio moyo wa kiungu ambao wazee wetu wa imani walikuwa nao.

Warumi 12:18-20 “Kama yamkini, kwa upande wenu, mkae katika amani na watu wote. Wapenzi, msijilipize kisasi, bali ipisheni ghadhabu ya Mungu; maana imeandikwa, Kisasi ni juu yangu mimi; mimi nitalipa, anena Bwana. Lakini, Adui yako akiwa na njaa, mlishe; akiwa na kiu, mnyweshe; maana ufanyapo hivyo, utampalia makaa ya moto kichwani pake.”                

Waebrania 12:14-15 “Tafuteni kwa bidii kuwa na amani na watu wote, na huo utakatifu, ambao hapana mtu atakayemwona Bwana asipokuwa nao; mkiangalia sana mtu asiipungukie neema ya Mungu; shina la uchungu lisije likachipuka na kuwasumbua, na watu wengi wakatiwa unajisi kwa hilo.”            

Na. Rev. Innocent Samuel Kamote.

Mkuu wa wajenzi mwenye Hekima.

Jumapili, 9 Novemba 2025

Dawa isiyoshindwa!


Yeremia 8:21-22 “Kwa sababu ya maumivu ya binti ya watu wangu nimeumia mimi; nimevaa kaniki; ushangao umenishika. Je! Hapana zeri katika Gileadi? Huko hakuna tabibu? Mbona, basi, haijarejea afya ya binti ya watu wangu?




Utangulizi:

Tuwapo duniani kama wanadamu wakati mwingine yako majeraha na maumivu ya mambo tunayokutana nayo katika maisha ambayo ni magumu kupona hususani majeraha ya moyoni, wako watu ambao wanaishi kwa mashaka, wamevunjika moyo, wamekosa amani, wamekata tamaa, wana misiba ya aina mbalimbali katika maisha na wengine wameumizwa na mioyo yao imejaa uchungu hakuna utulivu katika maisha yao, wamelia machozi mpaka wamechoka, hawawezi kutibiwa katika hali ya kawaida, hawawezi kusaidiwa na wanasaikolojia wala washauri nasaha, wanateseka, wana maumivu endelevu wana makovu, mashaka na mgandamizo wa mawazo wameshindwa kupata tiba ya kibinadamu inayoweza kuwasaidia, hakuna dawa, leo nawajulisha kuwa iko Dawa isiyoshindwa!

Nyakati za Biblia ilikuwepo dawa inayojulikana kama “Dawa isiyoshindwa” ambayo ilikuwa na uwezo wa kutuliza maumivu na kurejesha afya ya mtu aliyeumizwa dawa hii ilijulikana kama Zeri ya Gileadi, dawa hii Zeri ilikuwa inapatikana katika sehemu ya kaskazini Mashariki ya Israel katika bonde la mto Jordan, dawa hii ilikuwa inatumika kutibu na kufariji watu waliopatwa na maumivu na majeraha ya aina mbalimbali sugu, Dawa hii ilijipatia umaarufu mkubwa na ilikuwa ni moja ya bidhaa adimu sana.

Kwa hiyo ilikuwa kama mtu amejeruhiwa na kuumizwa, na kisha ikaonekana kana kwamba Jeraha lake haliponi na akahangaika kutumia dawa nyingi sana na zikigonga ukuta basi dawa ya mwisho ilipendekezwa kuwa Zeri kwa sababu, Zeri ilikuwa ni dawa isiyoshindwa kwa jitihada za kibinadamu.

Yeremia 46:11-12 “Panda uende Gileadi, ukatwae zeri, Ee binti, bikira wa Misri; unatumia dawa nyingi bure tu; hupati kupona kamwe. Mataifa wamesikia habari za aibu yako, nayo dunia imejaa kilio chako; maana shujaa amejikwaa juu ya shujaa mwenzake, wameanguka wote wawili pamoja.”

Leo basi tutachukua muda kuzungumzia kwa ufupi kuhusiana ana dawa hii isiyoshindwa iliyotumika kutibu majeraha sugu unhealed wounds or chronic wound iliyoitwa Zeri ya Gileadi kwa kuzingatia vipengele vya msingi vitatu vifuatavyo:-



·         Ufahamu kuhusu Zeri ya Gilead

·         Matumizi ya Zeri nyakati za Biblia

·         Dawa isiyoshindwa



Ufahamu kuhusu Zeri ya Gilead

Ni muhimu kufahamu kuwa Zeri nyakati za Biblia ulikuwa ni mmea ambao ulitumika kutengenezea viungo na mafuta yenye harufu nzuri ambayo yalitumika kutibu majeraha na vidonda sugu pamoja na maradhi mbalimbali yaliyoshindikana, Dawa hii ilipatikana katika eneo maarufu huko Jordani kaskazini mashariki mwa Israel katika bonde la mto Jordani ambako kulikuwa na misitu mizito yenye mimea ya dawa zenye thamani kubwa ukiwepo mmea huu uitwao Zeri ambao kwa Kiebrania unaitwa “Tsoriy”  na kwa kiingereza “Balm of Gilead”  Sifa mojawapo ya Zeri ilikuwa ni kutibu kwa haraka, kuleta faraja na urejesho wa uponyaji wa jeraha lililoshindikana, Kama mtu alikuwa anakuheshimu sana mojawapo ya zawadi ambayo angeweza kukuletea pamoja na viungo mbalimbali basi angeweza kukupatia na zeri katika zawadi zake, lakini moja ya biashara kubwa sana nyakati za agano la kale pamoja na mambo mengine ilikuwa ni  Zeri ambayo kimsingi inapatikana Gilead tu!

Mwanzo 37:23-25 “Ikawa Yusufu alipofika kwa ndugu zake, wakamvua Yusufu kanzu yake, kanzu ile ndefu aliyoivaa, wakamtwaa wakamtupa katika birika; na hiyo birika ilikuwa tupu, hamna maji. Nao wakakaa kitako kula chakula; wakainua macho yao, wakaona, msafara wa Waishmaeli wanakuja wakitoka Gileadi na ngamia zao, wakichukua ubani na zeri na manemane, wakisafiri kuvichukua mpaka Misri.”

Mwanzo 43:11-13 “Israeli, baba yao, akawaambia, Kama ndivyo, fanyeni hivi; twaeni tunu za nchi katika vyombo vyenu, mkamchukulie mtu huyo zawadi, zeri kidogo, na asali kidogo, ubani, na manemane, na jozi, na lozi. Mkatwae fedha maradufu mikononi mwenu, na fedha zile zilizorudishwa kinywani mwa magunia yenu zirudisheni mikononi mwenu; labda zilisahauliwa. Mtwaeni na ndugu yenu, mwondoke na kurudi kwa mtu yule.”

Matumizi ya Zeri nyakati za Biblia

Nyakati za Biblia ilikuwa kama mtu amepata majeraha na kuumia na kutibiwa kwa tiba za aina nyingine na tiba hizo zikashindikana kisha jeraha likachukua wiki zaidi ya nne mpaka sita bila kupona kwa matabibu wa kila aina basi shauri la mwisho kwa mgonjwa angeshauriwa apande kwenda Gilead kwani huko angeweza kupata tiba  ya zeri dawa isiyoshindwa ambayo ilijulikana kama zeri ya Gilead

Yeremia 8:21-22 “Kwa sababu ya maumivu ya binti ya watu wangu nimeumia mimi; nimevaa kaniki; ushangao umenishika. Je! Hapana zeri katika Gileadi? Huko hakuna tabibu? Mbona, basi, haijarejea afya ya binti ya watu wangu?

Yeremia 46:11-12 “Panda uende Gileadi, ukatwae zeri, Ee binti, bikira wa Misri; unatumia dawa nyingi bure tu; hupati kupona kamwe. Mataifa wamesikia habari za aibu yako, nayo dunia imejaa kilio chako; maana shujaa amejikwaa juu ya shujaa mwenzake, wameanguka wote wawili pamoja.”

Yeremia 51:6-8 “Kimbieni kutoka kati ya Babeli, kila mtu na ajiokoe nafsi yake; msikatiliwe mbali katika uovu wake; maana ni wakati wa kisasi cha Bwana, atamlipa malipo. Babeli umekuwa kikombe cha dhahabu mkononi mwa Bwana; kilicholevya dunia yote; mataifa wamekunywa mvinyo wake; kwa sababu hiyo mataifa wameingiwa na wazimu. Babeli umeanguka na kuangamia ghafula; mpigieni yowe; twaeni zeri kwa maumivu yake; ili labda apate kuponywa.”

Unaona nyakati za Biblia mtu alipokuwa anaugua na mauti ikaonekana inanyemelea maisha ya mgonjwa na kuiondolea familia faraja suluhu kubwa ilikuwa ni kwenda Gilead au kutafuita tabibu mwenye ujuzi wa kutibu kwa kutumia Zeri ili yamkini kuweza kurejesha afya ya muathirika, hii ilikuwa ni dawa isiyoshindwa ilikuwa ni suluhu na mwisho wa changamoto ya mtu, wagonjwa waliposikia Zeri imepatikana walirudisha matumaini wakijua ya kuwa uponyaji wao umepatikana kwani Zeri iliponya maumivu yao kwa haraka na kuwarejeshea matumaini, na kuwaondolea msongo wa mawazo  na mashaka ya wauguzaji na kilio cha waliokata tamaa kingefikia ukingoni, zeri ilirudisha mzunguko wa uhai wa damu, ingedhoofisha maambukizi, na kurejesha mfumo wa kinga kwa haraka! Na kuziponya seli zilizoanza kufa na kusababisha uponyaji ulikuwa ni mmea wa ajabu na wa faida.


Dawa isiyoshindwa

Kimsingi maandiko ya agano la kale yalikuwa yanatoa picha ya kinabii (metaphor) iliyokuwa ikimuonyesha Yesu Kristo kama dawa ya kweli isiyoshindwa, Yesu Kristo ndiye zeri ya Gilead, yeye ndiye mwenye uwezo wa kutibu, majeraha ya moyo na kuleta faraja kwa watu waliokosa tiba katika mazingira mengine ya kawaida, Zeri ya Gilead ilikuwa ikitoa unabii kivuli wa dawa halisi isiyoshindwa na ni dawa ya milele yenyewe inauwezo wa kuponya kila kilichoshindikana katika mazingira ya kawaida ya kibinadamu, Uponyaji uliotolewa na zeri ulikuwa ni uponyaji wa muda tu lakini uponyaji unaotolewa na Yesu Kristo ni uponyaji wa milele, Yesu sio tu anauwezo wa kuponya majeraha lakini pia ana uwezo wa kuponya mioyo iliyojerushiwa kwa dhambi na changamoto mbalimbali za maisha

Yesu Kristo ni tabibu wa roho zote zilizojeruhiwa, kama zeri iliponya mwili na maumivu yake Yeye Yesu Kristo ana uwezo wa kuponya mwili nafsi na roho na kufutilia mbali majeraha yote ya moyoni na uchungu wa aina mbalimbali, sio hivyo tu kila ugonjwa na changamoto zilizowakumba watu ambazo zilishindikana kwa matabibu wote zilipoletwa kwa Yesu Kristo ilikuwa ni kama mtu amepanda kwenda Gileaed  kwani angepokea uponyaji wake wa uzina huu bna ule ujao wa milele!

Luka 4:17-19 “Akapewa chuo cha nabii Isaya, akakifungua chuo, akatafuta mahali palipoandikwa, Roho wa Bwana yu juu yangu, Kwa maana amenitia mafuta kuwahubiri maskini habari njema. Amenituma kuwatangazia wafungwa kufunguliwa kwao, Na vipofu kupata kuona tena, Kuwaacha huru waliosetwa, Na kutangaza mwaka wa Bwana uliokubaliwa.”

Marko 5:25-29 “Na mwanamke mmoja mwenye kutoka damu muda wa miaka kumi na miwili, na kuteswa mengi kwa mikono ya matabibu wengi, amegharimiwa vitu vyote alivyo navyo, kusimfae hata kidogo, bali hali yake ilizidi kuwa mbaya aliposikia habari za Yesu, alipita katika mkutano kwa nyuma, akaligusa vazi lake; maana alisema, Nikiyagusa mavazi yake tu, nitapona. Mara chemchemi ya damu yake ikakauka, naye akafahamu mwilini mwake kwamba amepona msiba ule.”

1Petro 2:23-25 “Yeye alipotukanwa, hakurudisha matukano; alipoteswa, hakuogofya; bali alijikabidhi kwake yeye ahukumuye kwa haki. Yeye mwenyewe alizichukua dhambi zetu katika mwili wake juu ya mti, tukiwa wafu kwa mambo ya dhambi, tuwe hai kwa mambo ya haki; na kwa kupigwa kwake mliponywa. Kwa maana mlikuwa mnapotea kama kondoo; lakini sasa mmemrudia Mchungaji na Mwangalizi wa roho zenu.”

Je hapana zeri katika Gilead? Je hakuna tabibu huko? Mbona watu wanaumia mbona watu hawaponi? Ni kwa sababu watu hawataki wenyewe kuja kwa Yesu, kama watu wa Mungu watajinyenyekesha na kutubu  na kuacha njia zao mbaya uponyaji upo na unawasubiria watu wa Mungu, tunatoa wito kwa watu wote waliojeruhiwa na wenye maumivu waje kwa Yesu kwa uponyaji yeye ni dawa ya kweli yeye ni dawa isiyoshindwa!

2Nyakati 7:13-15 “Nikizifunga mbingu isiwe mvua, tena nikiamuru nzige kula nchi, au nikiwapelekea watu wangu tauni; ikiwa watu wangu, walioitwa kwa jina langu, watajinyenyekesha, na kuomba, na kunitafuta uso, na kuziacha njia zao mbaya; basi, nitasikia toka mbinguni, na kuwasamehe dhambi yao, na kuiponya nchi yao. Sasa macho yangu yatafumbuka, na masikio yangu yatasikiliza maombi ya watu waombao mahali hapa.”

Ni tabibu wa karibu, tabibu wa ajabu! Tenzi Na:7


Na. Rev. Innocent Samuel Kamote.

Mkuu wa wajenzi mwenye Hekima

Alhamisi, 6 Novemba 2025

Msifungiwe nira pamoja na wasioamini


2Wakorintho 6:14-18. “Msifungiwe nira pamoja na wasioamini, kwa jinsi isivyo sawasawa; kwa maana pana urafiki gani kati ya haki na uasi? Tena pana shirika gani kati ya nuru na giza? Tena pana ulinganifu gani kati ya Kristo na Beliari? Au yeye aaminiye ana sehemu gani pamoja na yeye asiyeamini? Tena pana mapatano gani kati ya hekalu la Mungu na sanamu? Kwa maana sisi tu hekalu la Mungu aliye hai; kama Mungu alivyosema, ya kwamba, Nitakaa ndani yao, na kati yao nitatembea, nami nitakuwa Mungu wao, nao watakuwa watu wangu. Kwa hiyo, Tokeni kati yao, Mkatengwe nao, asema Bwana, Msiguse kitu kilicho kichafu, Nami nitawakaribisha.Nitakuwa Baba kwenu, Nanyi mtakuwa kwangu wanangu wa kiume na wa kike,”




Utangulizi:

Mojawapo ya fundisho muhimu sana katika maisha ya Ukristo ni pamoja na fundisho hili Msifungiwe nira pamoja na wasioamini! Fundisho hili kimsingi linawaonya wakristo kutokuwa na ushirika wa karibu sana na mtu asiyeamini, uhusiano huu ni ule unaoweza kuathiri uhusiano wetu tulio nao na Mungu, hii ikiwa na maana ya ushirikiano wa kibiashara, kindoa, uchumba na urafiki wa karibu wenye ushawishi mkubwa wa kimaadili na kimwenendo! Pamoja na maswala ya kiibada au maswala ya kiroho. Kimsingi kuna aina ya maisha ambayo wakristo tunapaswa kuyaishi katika mazingira ya maisha yetu ambayo yatasababisha uhusiano wetu na Mungu kuwa wa karibu na wa kudumu.

2Wakorintho 6:17-18 “Kwa hiyo, Tokeni kati yao, Mkatengwe nao, asema Bwana, Msiguse kitu kilicho kichafu, Nami nitawakaribisha. Nitakuwa Baba kwenu, Nanyi mtakuwa kwangu wanangu wa kiume na wa kike,”

Leo tutachukua muda kujifunza somo hili la msingi na la muhimu sana katika maisha ya wokovu Msifungiwe nira pamoja na wasioamini kwa kuzingatia vipengele vikuu muhimu vitatu vifuatavyo:-


·         Maana ya kufungiwa Nira.

·         Madhara ya kufungiwa Nira na wasioamini.

·         Faida za kutokufungiwa Nira na wasioamini.


Maana ya kufungiwa Nira

2Wakorintho 6:14-15 “Msifungiwe nira pamoja na wasioamini, kwa jinsi isivyo sawasawa; kwa maana pana urafiki gani kati ya haki na uasi? Tena pana shirika gani kati ya nuru na giza? Tena pana ulinganifu gani kati ya Kristo na Beliari? Au yeye aaminiye ana sehemu gani pamoja na yeye asiyeamini?

Ni muhimu kuwa na ufahamu wa kutosha kuhusiana na somo hili, ili hatimaye tuweze kuyatumia maandiko haya kwa faida ya ufalme wa Mungu bila kuathiri uwepo wetu katika jamii, jambo la msingi na la muhimu kwanza ni kuhakikisha ya kuwa tunakuwa na ufahamu wa maana ya neno “Nira”, Neno Nira katika Lugha ya Kiebrania linasomeka kama neno “Motah” na katika lugha ya kiyunani linasomeka kama neno “Zygos” yote yakiwa na maana ya kifaa cha mbao au cha chuma kinachofungwa au kuwekwa juu ya shingo za wanyama wawili wanaofanana wa kazi ili waweze kufanya kazi kwa pamoja aidha ya kulima au kuvuta mzigo, kwa kiingereza “Yoke”, lakini katika maana ya kiroho neno hili linamaanisha kufanya agano, au kuingia mkataba wa ushirika wa karibu sana na mtu, nchi, biashara au ndoa, au patano au agano kwa hiyo kufungiwa nira ni uhusiano wa karibu sana na mtu mwingine ili kushirikiana katika maswala nyeti na ya ndani kiimani, kimaisha, kindoa, kibiashara au ushirika wa kiroho au udhamini, au kupana mikono, au kuambatana, au kutoa udhamini wa kisheria mahakamani. Ushirika wa aina hii kimaandiko umekatazwa na tunaonywa kujihadhari nao kwa gharama yoyote ile kwa faida yetu! Na kwa faida ya ushirika wetu na Mungu.

Agizo la kutokufungiwa nira katika andiko hili maana yake ni maneno ya fumbo “metaphor” lenye kumaanisha kuwa mtu anayemuamini Mungu ni tofauti na mtu asiyemuamini Mungu na kwa sababu hiyo hawawezi kutekeleza lengo moja lenye kumuhusisha Mungu kwa pamoja, Mtu alieyemuamini Mungu ni kama na mnyama kazi aliyefundishwa kufanya kazi, na yule asiyeamini ni kama mnyama asiyefundishwa kufanya kazi kwa hiyo lengo la kuifanya kazi iliyokusudiwa haiwezi kutimia au kufikia malengo ni sawa na kuvalishwa Nira kwa wanyama wa aina mbili tofauti jambo ambalo linaweza kusababisha maumivu kwa mmoja kwa sababu hawalingani uwezo na hawafanani  na nguvu zao pia haziko sawa! Au umri wa wanyama kazi hao au vimo vyao vinatofautiana sana! Na hivyo kum-athiri mwingine

Walawi 19:19 “Mtazishika amri zangu. Usiwaache wanyama wako wa mfugo wakazaana kwa namna mbalimbali; usipande shamba lako mbegu za namna mbili pamoja; wala usivae mwilini mwako nguo ya namna mbili zilizochanganywa pamoja.”

Kumbukumbu 22:9-10 “Usipande shamba lako la mizabibu aina mbili za mbegu; yasije yakaondolewa matunda yote, mbegu ulizopanda na maongeo ya mizabibu yako. Usilime kwa ng'ombe na punda wakikokota jembe pamoja.”

Zaburi 1:1-3 “Heri mtu yule asiyekwenda Katika shauri la wasio haki; Wala hakusimama katika njia ya wakosaji; Wala hakuketi barazani pa wenye mizaha. Bali sheria ya Bwana ndiyo impendezayo, Na sheria yake huitafakari mchana na usiku. Naye atakuwa kama mti uliopandwa Kandokando ya vijito vya maji, Uzaao matunda yake kwa majira yake, Wala jani lake halinyauki; Na kila alitendalo litafanikiwa.”

Watu walioamini ni aina nyingine ya mbegu na haiwezi kuchanganywa na watu wasioamini, ambao ni mbegu nyingine, watu wa Mungu hawawezi kuwa na ushirika wa karibu au wa kiagano au wa kiibada au wa kindoa na watu wasioamini, kuwaunganisha hivyo ni sawa na kuweka wanyamakazi Punda na Ng’ombe ambao kimsingi hawafanani wala hawalingani na hawawezi kufanya kazi moja kwa pamoja,  na sio haki kuwafunganisha pamoja, watu waaminio wana sheria na wasioamini hawana sheria, waaminio wanaishi kwa maelekezo ya Mungu wasioamini wanaishi watakavyo, walioamini wanajifunza na kufundishwa namna na jinsi ya kutembea na Mungu wasioamini ni tofauti wanafuata kawaida ya ulimwengu huu kwa hiyo hakuna ulinganifu wa kimzani kati ya mtu aliyemuamini Mungu na yule asiyeamini. Mmoja ni hekalu la Mungu mwingine ni hekalu la sanamu, hii ni lugha ya hali ya juu na ya ndani yenye kusisitiza utofauti ulioko kati ya mtu aliyeokoka na mtu asiyeokoka, aaminiye na asiyeamini, lugha zinazotumika kuelezea ushirika huu katika kiingreza “Be ye not unequally yoked together with unbelievers” kisha kuna maneno fellowship, communion, concord, part, agreement. kwa hiyo kuna maneno unequally, fellowship, communion, concord, part, agreement ambayo katika kiyunani yanasomeka kama Heterozugeo, (Associate), Motechē (Participation or intercourse), sumphonēsis (Concord, Harmony, a state of agreement), Meris (Share, Patakers), sugkatathesis – soong-kat-ath’-es-is (in company) kwa hiyo ukiyaangalia maneno hayo yote yanayotumika katika kifungu hiki cha 2Wakorintho 6:14-18 yanamaanisha kuwa hatupaswi kamwe kuambatana, kushirikiana, kuingiliana, kukubaliana nao, kushirikisha, kufanya urafiki, kufanya kazi moja, kuchanganyika nao katika jambo moja mfano kama vyombo vya muziki vinapopigwa gitaa, ngoma, na kinanda, kisha vikatoa mziki wa aina moja, “a simultaneous cccurence of two or more musical tones that produce an impression of agreeableness or resolution on a listener” kwa hiyo wakristo wanapofanya ushirika wa aina hii unaokatazwa na maandiko yanatufundisha kuwa kitakachotokea kitaalamu kinaitwa “DISCORD” – “a lack of agreement or harmony as between persons, things or ideas, active quarrelling or conflict resulting from discord among person or function” “harsh or unpleasant sound” hali itakayozalishwa itakuwa ni kelele za kutokukubaliana, kutokufikia muafaka, kupingana kimawazo na kimtazamo, kutokea kwa migogoro na ugomvi, kukosekana kwa amani na utulivu, kukosekana kwa utaratibu na ustaarabu, ugomvi endelevu, chuki na sauti zisizopendeza,  kwa sababu hiyo uwepo wa Mungu hauwezi kuwepo mahali pa namna hiyo  ni mpaka mtu wa Mungu ajiondoe kwenye patano la aina hiyo.

Nira huwaunganisha wanyama wawili wa aina moja na kuwafanya wafanye kazi moja wanyama hao ni kama ng’ombe kwa ng’ombe na punda kwa punda, Wanyama hao wanapokuwa hawafanani kuna uwezekano mkubwa wa kuumizana  na kumuathiri mmoja kwani wanaweza kuwa na tofauti ya nguvu na kimo, (horse power) Nguvu ya punda na ng’ombe zinatofautiana, aidha hata kiumri wakati mwingine wanatakiwa kufanana kama, hawafanani kunakuweko uwezekano mkubwa wa kuifanya kazi isiwe na ufanisi au kazi inakuwa ngumu sana na kusababisha maumivu na makwazo kwa kila mmoja. Lakini mbaya zaidi ni kuondoa uwepo wa Mungu, kwa hiyo agizo la Msifungiwe nira na wasioamini lina faida kubwa sana kwa Mkristo, mtu wa Mungu, kuliko tunavyoweza kufikiri.  Kwa hiyo hata mtu aliyeokoka akishiriki mapenzi na mtu asiyeokoka ni sawa na kuchukua viungo vya Kristo na kuvifanya vya kahaba

1Wakorintho 6:15-17 “Je! Hamjui ya kuwa miili yenu ni viungo vya Kristo? Basi nivitwae viungo vya Kristo na kuvifanya viungo vya kahaba? Hasha! Au hamjui ya kuwa yeye aliyeungwa na kahaba ni mwili mmoja naye? Maana asema, Wale wawili watakuwa mwili mmoja.  Lakini yeye aliyeungwa na Bwana ni roho moja naye.”   

Amosi 3:3 “Je! Watu wawili waweza kutembea pamoja, wasipokuwa wamepatana?

Neno la Mungu hapo linaonya kutokuingia katika ushirika wa karibu au uhusiano wa ndani sana na kujifunga na watu mnaotofautiana kiimani au hata kimafundisho, kimsingi tunaonywa kutokuchukuliana na wasioamini katika imani kwani imani yao na uadilifu wao na akili zao ni tofauti na kwa sababu hiyo upande mmoja unaweza kusababishiwa makwazo, majuto, maumivu na machungu na kuondoa ufanisi katika utii na uchaji wa Mungu. Hii haimaanishi kutokuweko kabisa duniani, au kutokushirikiana na watu wa dunia hii katika kuleta maendeleo, hapana bali neno la Mungu hapa linatoa tahadhari ya kutokujifunga kiagano, kipatano na kirafiki, na ushawishi na walimwengu kwani kimsingi badala ya wewe kuwavuta na kuwashawishi wewe mtu wa Mungu ndiye unayeweza kuathiriwa. “Believers should not be in close partnership with non- believers” Waamini hawapaswi kuwa na ushirika wa karibu na wasioamini. Ili kuwaepushia na madhara yanayoweza kuumiza mioyo yao na kupoteza ushirika na uwepo wa Mungu.

Madhara ya kufungiwa Nira na wasioamini.

Biblia iko makini sana na ushirikiano wa kiroho na muungano wa kiroho na agano la kiroho kati ya watu waaminio na wasioamini, kwa sababu Mungu anajua wazi kuwa kuna madhara makubwa sana katika muungano huo na shughuli zake haziwezi kwenda kwa ufanisi unaohitajika, ili Mungu atembee katikati yetu kwa uhuru na Baraka, Kimsingi hakuna kitu kinaweza kumzuia Mungu kutekeleza kutimiza kusudi, lake hata hivyo kwa kanuni ya neno lake Mungu ni kwamba kutofungiwa nira kuna:-

a.       Kuepusha migogoro ya kimaadili na kiimani – Watu wasioamini hawana Msingi wa Neno la Mungu, sawa na mnyama asiyefunzwa au kuandaliwa kama mnyama kazi na hivyo mtazamo wao kuhusu Ndoa, Biashara au maisha ya kiroho unapingana na ule msimamo wa maelekezo ya neno la Mungu, kwa sababu hiyo neno la Mungu linaagiza kwa ukali kuacha mahusiano nao, kwa maana nyingine kufanya maamuzi magumu ya kujiepusha nao (kuua, au kukata). Kuvunja na kuharibu kabisa mahusiano na wale wanaoweza kukukosesha.

 

Kumbukumbu 13:6-10 “Atakapokushawishi kwa siri ndugu yako, mwana wa mamaako, au mwana wako, au binti yako, au mke wa kifuani mwako, au rafiki yako aliye kama moyo wako, akikuambia, Twende tukaabudu miungu mingine usiyoijua wewe wala baba zako; katika miungu ya mataifa yaliyo kando-kando yenu karibu nawe au mbali nawe, tokea ncha moja ya dunia hata ncha ya pili ya dunia; usimkubalie wala usimsikize; wala jicho lako lisimwonee huruma, wala usimwache, wala usimfiche; mwue kweli; mkono wako na uwe wa kwanza juu yake katika kumwua, na baadaye mikono ya watu wote. Nawe mtupie mawe hata afe; kwa kuwa alitaka kukupotoa na Bwana, Mungu wako aliyekutoa katika nchi ya Misri, katika nyumba ya utumwa.”

 

Mathayo 18:8-9 “Basi mkono wako au mguu wako ukikukosesha, ukate ukautupe mbali nawe; ni afadhali kuingia katika uzima hali umepungukiwa na mkono au mguu, kuliko kuwa na mikono miwili au miguu miwili, na kutupwa katika moto wa milele. Na jicho lako likikukosesha, ling'oe, ukalitupe mbali nawe; ni afadhali kuingia katika uzima una chongo, kuliko kuwa na macho mawili, na kutupwa katika jehanum ya moto.”

                 

Maandiko yanatumia lugha ya mkazo au mkuzo kitaalamu inaitwa “Hyperbole” kufundisha au kusisitiza msimamo mkali (Radical Action) kuhusiana na maisha ya dhambi na madhara yake, kwa hiyo katika maandiko hayo juu, maana yake sio katika uhalisia wa lugha iliyotumika lakini ni kuchukua hatua madhubuti au kufanya maamuzi magumu ya mabadiliko ya kitabia au kijamaa au kirafiki na watu wanaokukosesha au wenye kukupa ushawishi kuelekea katika maisha ya dhambi, ni afadhali kuua urafiki huo au ni afadhali urafiki huo ufe kuliko kuwa na mtu au watu au ushirika unaokufanya uende motoni, kwa hiyo Musa anaposema ndugu yako akikushawishi muue, na Yesu anaposema mkono wako au mguu wako ukikukosesha uukate wote wanaanisha kufanya maamuzi magumu kwaajili ya uzima wa milele kuliko kuchukuliana (Compromising) ambako kutakusababishia uende jehanamu ya moto kwa hiyo fundisho la kutokufungiwa nira hali kadhalika ni mkazo wa kufanya maamuzi magumu kujiondoa au kujitoa katika ushirika unaotushawishi kuishi maisha ya dhambi na yenye tofauti za kimtazamo na kiitikadi. Nuru na giza, au haki na uasi. Kwa hiyo neno la Mungu linatutaka tuache uhusiano unaotupelekea kumkosea Mungu au kujitia unajisi.

 

Waebrania 12:3-4 “Maana mtafakarini sana yeye aliyeyastahimili mapingamizi makuu namna hii ya watendao dhambi juu ya nafsi zao, msije mkachoka, mkizimia mioyoni mwenu. Hamjafanya vita hata kumwagika damu, mkishindana na dhambi;”

 

b.      Huduma na maisha ya Imani hudhoofika – Kufungiwa nira na wasioamini kunasababisha mtu akosane na Mungu na Mungu asitembee pamoja naye, Huduma ya mtu aliyefungiwa nira na wasioamini hudhoofika na kumfanya mtu kudhoofika kiimani na kihuduma na kuwa mbali na Mungu, au badala ya kumtumikia Mungu kwa furaha na moyo mweupe unaishi maisha ya maumivu mengi, kurudi nyuma kukwazwa, kudhoofishwa, kuchukizwa, kukosa amani na kukata tamaa badala ya kutiwa moyo, kuambatana na kushikamana na watu wa Mungu kunaleta uchochezi mkubwa wa kusonga mbele katika maisha ya wokovu na ustawi badala ya kudhoofika na kusinyaa au kupoa. Jambo hili linapunguza uwepo wa Mungu katika maisha yetu, Mfalme Suleimani aliyekuwa anampenda Mungu kiasi cha kutokewa na Mungu mara mbili katika maisha yake na kupewa akili na hekima nyingi kuliko mtu yeyote kbla yake au baada yake alipoa sana kiroho kiasi cha kuabudu miungu mingine kutokana na kushikamana na wake zake na kuwasikiliza na kuwatii ili kuwapendeza na wakamfanya apoe kiroho na kuabudu miungu mingine jambo ambalo lilimuhuzunisha sana Mungu!.

 

2Wakorintho 6:17-18.“Kwa hiyo, Tokeni kati yao, Mkatengwe nao, asema Bwana, Msiguse kitu kilicho kichafu, Nami nitawakaribisha. Nitakuwa Baba kwenu, Nanyi mtakuwa kwangu wanangu wa kiume na wa kike,”

 

1Wafalme 11:1-4 “Mfalme Sulemani akawapenda wanawake wengi wageni, pamoja na binti yake Farao, wanawake wa Wamoabi, na wa Waamoni, na wa Waedomi, na wa Wasidoni, na wa Wahiti, na wa mataifa Bwana aliyowaambia wana wa Israeli, Msiingie kwao, wala wasiingie kwenu; kwa kuwa hakika wataigeuza mioyo yenu kuifuata miungu yao. Sulemani akaambatana nao kwa kuwapenda. Akawa na wake mia saba binti za kifalme, na masuria mia tatu; nao wakeze wakamgeuza moyo. Maana ikawa, Sulemani alipokuwa mzee, wake zake wakamgeuza moyo wake, afuate miungu mingine, wala moyo wake haukuwa mkamilifu kwa Bwana, Mungu wake, kama moyo wa Daudi baba yake.”

 

c.       Kufanyika mtego na mjeledi kwa watu wa Mungu - Mungu aliwaonya Israel kuwa endapo wataungana na wenyeji na kuoana na watu hawa wasiomcha Mungu watu hao watakuwa mtego kwao, watakuwa kwazo na mtego na mzigo mzito shingoni mwao, lakini pia watakuwa mjeledi yaani watasababisha maumivu makali katika maisha yao watakuwa miiba, na Mungu hatawaondoa, itakuwa kama adhabu ya ukaidi kinyume na agizo la Mungu. Kwa ujumla kumpenda Mungu kunaenda sambamba na kujitenga na uovu na watu waovu

 

Yoshua 23:11-13 “Jihadharini nafsi zenu, basi, ili mmpende Bwana, Mungu wenu. Lakini mkirudi nyuma kwa njia yo yote na kushikamana na mabaki ya mataifa, yaani, mataifa haya yaliyobaki kati yenu, na kuoana nao, na kuingia kwao, nao kuingia kwenu; jueni hakika ya kuwa Bwana, Mungu wenu, hatawafukuza tena mataifa haya mbele ya macho yenu, bali watakuwa mtego kwenu na tanzi, na mjeledi mbavuni mwenu, na miiba machoni mwenu, hata mtakapoangamia na kutoka katika nchi hii njema, ambayo Bwana, Mungu wenu, amewapa ninyi.”       

 

Kumbukumbu 7:1-6 “Bwana, Mungu wako, atakapokutia katika nchi uendayo kuimiliki, atakapoyang'oa mataifa mengi watoke mbele yako, Mhiti, na Mgirgashi, na Mwamori, na Mkanaani, na Mperizi, na Mhivi, na Myebusi, mataifa saba makubwa yenye nguvu kukupita wewe; wakati Bwana, Mungu wako, atakapowatoa mbele yako, nawe utawapiga; wakati huo ndipo uwaondoe kabisa; usifanye agano nao, wala kuwahurumia; wala usioane nao; binti yako usimpe mwanawe mume, wala usimtwalie mwanao mume binti yake. Kwa kuwa atamkengeusha mwanao mume asinifuate, ili wapate kuabudu miungu mingine; ndipo itakapowaka hasira ya Bwana juu yenu, naye atakuangamiza upesi. Lakini watendeni hivi; zivunjeni madhabahu zao zibomosheni nguzo zao, yakateni maashera yao, ziteketezeni kwa moto sanamu zao za kuchonga. Kwa maana wewe u taifa takatifu kwa Bwana, Mungu wako; Bwana Mungu wako, amekuchagua kuwa watu wake hasa, zaidi ya mataifa yote walioko juu ya uso wa nchi.”

 

Ezra 9:10-12. “Na sasa, Ee Mungu wetu, tuseme nini baada ya hayo? Maana tumeziacha amri zako, ulizoziamuru kwa midomo ya watumishi wako, manabii, ukisema, Nchi ile, mnayoiendea ili kuimiliki, ni nchi ya uchafu, kwa sababu ya uchafu wa watu wa nchi zile, kwa ajili ya machukizo yao, yaliyoijaza tangu upande huu mpaka upande huu, kwa uchafu wao. Basi, msiwape wana wao binti zenu, wala msitwae binti zao kuwa wake za wana wenu, wala msiwatakie amani wala kufanikiwa milele; ili mpate kuwa hodari, na kula wema wa nchi hiyo, na kuwaachia watoto wenu iwe urithi wa milele.”

               

Nehemia 13:23-26 “Tena siku zizo hizo nikawaona wale Wayahudi waliokuwa wameoa wanawake wa Ashdodi, na Amoni, na Moabu; na watoto wao wakanena nusu kwa lugha ya Ashdodi, wala hawakuweza kunena kwa Kiyahudi, bali kwa lugha ya watu hao mojawapo. Nikagombana nao, nikawalaani, nikawapiga baadhi yao, na kuwang'oa nywele zao; nikawaapisha kwa Mungu, nikasema, Msiwaoze wana wao binti zenu, wala msiwatwae binti zao ili waolewe na wana wenu, wala na ninyi wenyewe. Je! Sulemani, mwana wa Daudi, hakufanya dhambi kwa kutenda hayo? Lakini katika mataifa mengi hapakuwa na mfalme mwingine mfano wake. Tena alipendwa na Mungu wake, naye Mungu akamfanya mfalme juu ya Israeli; walakini wanawake wageni walimkosesha hata yeye.”

 

Vifungu hivi vyote vinatukumbusha wazi kuwa watu wa Mungu ni tofauti na watu wa dunia hii, watu wa Mungu wana utamaduni wao, utamaduni wao ni neno la Mungu, mtu wa dunia hii anaweza kujiunga na utamaduni huo kwa kuokoka, au kwa kuona na kuvutiwa na maisha yetu ambayo ni nuru ndani ya Kristo, kwa kweli jaribio lolote la kuwaoa au kuoana nao na kutarajia mabadiliko kutoka kwao ambayo hayatokani na Mungu kunaweza kuwa mtego kwetu na kwa watoto wetu, Musa aliliona hilo na Nehemia na Ezra pia walilikemea na Paulo anatukumbusha juu ya maamuzi haya Nehemia anawakumbusha Israel kuwa huwezi kutumia Hekima, kwani hata mtu mwenye Hekima aliyependwa na Mungu yaani Suleimani alibadilishwa moyo kwa mtego huu, Mungu anamtarajia mtu wake kuwa tofauti na watu wa dunia hii, na kutokuishi sawa na watu wa dunia hii wasiojali sheria na maadili ya kiungu ambayo ni Muhimu kwa uwepo wa Mungu, hii haina maana ya kuwa Mungu ni mbaguzi la hasha hata kidogo, lakini Mungu anataka kupitia sisi watu wa mataifa yote wageuzwe moyo na kumuelekea Mungu aliye hai na wa kweli.

 

Mathayo 5:14-16 “Ninyi ni nuru ya ulimwengu. Mji hauwezi kusitirika ukiwa juu ya mlima. Wala watu hawawashi taa na kuiweka chini ya pishi, bali juu ya kiango; nayo yawaangaza wote waliomo nyumbani. Vivyo hivyo nuru yenu na iangaze mbele ya watu, wapate kuyaona matendo yenu mema, wamtukuze Baba yenu aliye mbinguni.”                

 

d.      Kuzuia ukuaji wako wa kiroho – Kufungiwa nira pamoja na wasioamini hukufunga wewe katika hali yako ya kiroho na kuzuia ukuaji wako wa kiroho, Mtu aaminiye anapounganishwa na asiyeamini ushawishi wake wa kiroho unaathiriwa na kukengeushwa kwa ujumla kunakuwa na ugumu mkubwa kuishi maisha ya kumuheshimu Mungu, Mtu aliyeokoka anamwamini Kristo, Mtu asiyeokoka anamwamini Beliari, ubaradhuli, Mtu aliyeamini ni Hekalu la Mungu, mtu asiyeamini ni Sanamu, Mtu aliyeamini ni Nuru, mtu asiyeamini ni Giza, hawa ni wanyama wasiofanana hawawezi kwenda pamoja maumivu makali sana yatatokea, watu wengi waliokiuka kanuni hii wameumia sana, hakuwezi kuwako mafanikio ya kiroho na mafanikio ya kihuduma kwa watu ambao wamefungiwa Nira na wasioamini hakuna patano! Hapo wala hakuna shirika!

 

2Wakorintho 6:14-16 “Msifungiwe nira pamoja na wasioamini, kwa jinsi isivyo sawasawa; kwa maana pana urafiki gani kati ya haki na uasi? Tena pana shirika gani kati ya nuru na giza? Tena pana ulinganifu gani kati ya Kristo na Beliari? Au yeye aaminiye ana sehemu gani pamoja na yeye asiyeamini? Tena pana mapatano gani kati ya hekalu la Mungu na sanamu? Kwa maana sisi tu hekalu la Mungu aliye hai; kama Mungu alivyosema, ya kwamba, Nitakaa ndani yao, na kati yao nitatembea, nami nitakuwa Mungu wao, nao watakuwa watu wangu.”

                               

e.      Kuharibika kwa tabia njema – 1Wakorintho 13:33-34 “Msidanganyike; Mazungumzo mabaya huharibu tabia njema. Tumieni akili kama ipasavyo, wala msitende dhambi; kwa maana wengine hawamjui Mungu. Ninanena hayo niwafedheheshe.”

 

Kanuni ya kutokufungiwa nira na wasioamini pia inakwenda kugusa urafiki wa karibu, kuingia katika kufanya biashara au kuingia katika agano au kumdhamini mtu muovu waamini wanaaswa na maandiko kujihadhari kwani inaweza kukuweka matatani katika maswala ya imani yako kinyume na wasioamini, Neno mazungumzo mabaya katika Biblia ya kiingereza yanasomeka “Bad Company” neno la kiyunani linalotumika hapo ni “Homilia” ambalo ni sawa na neno la kiingereza “Companionship” au “intercourse” hii ikiwa na maana ya ushirika wa karibu na mtu muovu au watu waovu unamchango mkubwa sana katika kuharibu tabia njema, kwa hiyo waaminio hawapaswi kamwe kuwa na ukaribu wa kina na watu wenye ushawishi wa kutenda uovu, au wenye tabia mbaya ondoa watu wote wenye kusudi tofauti na lako kwa Mungu. 

 

Mithali 1:10-16 “Mwanangu, wenye dhambi wakikushawishi, Wewe usikubali. Wakisema, Haya! Njoo pamoja nasi, Na tuvizie ili kumwaga damu; Tumwotee asiye na hatia, bila sababu; Tuwameze hai kama kuzimu, Na wazima, kama wao washukao shimoni. Tutapata mali yote ya thamani, Tutazijaza nyumba zetu mateka.Wewe utashirikiana nasi; Tutakuwa na vitu vyote shirika. Mwanangu, usiende njiani pamoja nao; Uzuie mguu wako usiende katika mapito yao.”

 

f.        Kulinda utamaduni wa kikanisa – Kanisa ni chombo chenye utamaduni wake, tabia na maisha na mwenendo wetu ni tofauti na watu wa dunia hii, kufungiwa nira na wasioamini kunauwa utamaduni wa kanisa na kulifanya kanisa kupoteza ushawishi wake duniani, unaposoma yale yaliyomkuta Nehemia utagundua kuwa Mungu alikuwa na Mpango wa kulitunza Taifa la Israel ili liweze kuwa taifa la mfano na liwe Baraka kwa ulimwengu, kusudi hilo hilo limeletwa kwa kanisa, Kanisa leo limekuwa na utamaduni mchanganyiko kama ilivyokuwa kwa Israel, tabia nyingi sana zisizo za kiadilifu zimeingia makanisani, kuna kanisa moja katika mji fulani nilifika na kukuta hakuna mikesha huko, na kiongozi wa mahali hapo akaniambia anaogopa kufanya mikesha kwa sababu mikesha hiyo inatumiwa na vijana kufanya uovu, mikesha ni njia ya kanisa kupata muda mrefu wa kuomba pamoja lakini kama kanisa linafikia hatua ya kuogopa kukesha kwa sababu ya uasherati basi hakuna tofauti na wale wanaokwenda kukesha katika disco na ngoma utamaduni wa kumtafuta Bwana umetoweka, utamaduni wa kumcha Mungu na kuutafuta uso wake kwa bidi umetoweka na tabia za ajabu zimaingia, lugha na mwenendo umeathiriwa na mchanganyiko mkubwa wa kitabia umeingilia kati.  

 

Nehemia 13:23-25 “Tena siku zizo hizo nikawaona wale Wayahudi waliokuwa wameoa wanawake wa Ashdodi, na Amoni, na Moabu; na watoto wao wakanena nusu kwa lugha ya Ashdodi, wala hawakuweza kunena kwa Kiyahudi, bali kwa lugha ya watu hao mojawapo. Nikagombana nao, nikawalaani, nikawapiga baadhi yao, na kuwang'oa nywele zao; nikawaapisha kwa Mungu, nikasema, Msiwaoze wana wao binti zenu, wala msiwatwae binti zao ili waolewe na wana wenu, wala na ninyi wenyewe.”

 

1Petro 2:9-10 “Bali ninyi ni mzao mteule, ukuhani wa kifalme, taifa takatifu, watu wa milki ya Mungu, mpate kuzitangaza fadhili zake yeye aliyewaita mtoke gizani mkaingie katika nuru yake ya ajabu; ninyi mliokuwa kwanza si taifa, bali sasa ni taifa la Mungu; mliokuwa hamkupata rehema, bali sasa mmepata rehema.”

 

Warumi 12:2 “Wala msiifuatishe namna ya dunia hii; bali mgeuzwe kwa kufanywa upya nia zenu, mpate kujua hakika mapenzi ya Mungu yaliyo mema, ya kumpendeza, na ukamilifu.”

 

Kanisa ni taifa ni mzao mteule ni ukuhani wa kifalme, ni taifa takatifu, ni wtu wa miliki ya Mungu, Mungu amelitenga kanisa na dunia kwa sababu hiyo ni lazima kanisa likae katika utamaduni wake, kufungiwa nira na wasioamini kutalifanya kanisa kupoteza utaifa wake na utamaduni wake kwa hiyo badala ya waamini kuchukuliwa na tamaduni za ulimwengu huu, maandiko yanasisitiza kutokuenenda kwa viwango vya watu wa dunia hii, kwa hiyo ni lazima tujitoe kwa ukamilifu kwa Mungu  na kuyatoa maisha yetu kwake na kujihadhari sana na kujaribu kufuata tamaduni za ulimwengu huu, Mungu anataka iwe hivyo kwa wake zetu, waume zetu na watoto tutakaowazaa baadae wote waifuate njia ya Mungu na neno lake, sasa tukikubali kufungiwa nira tutapoteza hilo utamaduni wa kibiblia na wa kikanisa ambao Mungu ametuandaa sisi kuwa watu wa tofauti. Kumbuka wakati Israel waliposhuka Misri, Mungu aliugusa moyo wa Farao kuwapa nchi ya Gosheni, ili wasichangamane na Wamisri, kwani tamaduni zao zilikuwa tofauti na wamsiri hawachangamani na wafugaji jambo hili lilisaidia katiia kuwafanya Israel kuwa taifa la kipekee waliokuwa na kuongezeka katika inchi ya Misri, na kuwa na utamaduni wao na bila ya kupoteza utaifa wao na upekee wao kama Waebrania.

 

Mwanzo 46:31-34 “Yusufu akawaambia ndugu zake na watu wa nyumbani mwa baba yake, Nitapanda mimi nimpashe Farao habari; nitamwambia, Ndugu zangu, na watu wa nyumbani mwa baba yangu, waliokuwa katika nchi ya Kanaani, wamenijia. Na watu hao ni wachungaji, maana wamekuwa watu wa kuchunga wanyama, nao wameleta kondoo zao, na ng'ombe zao, na yote waliyo nayo. Itakuwa Farao atakapowaita, na kuwauliza, Kazi yenu ni nini? Semeni, Watumwa wako tumekuwa wachunga wanyama tangu ujana wetu, na hata leo, sisi, na baba zetu; mpate kukaa katika nchi ya Gosheni; maana kila mchunga wanyama ni chukizo kwa Wamisri.”

Faida za kutokufungiwa Nira na wasioamini

Paulo anapotukumbusha au kuwakumbusha Wakorintho kutokufungiwa Nira na wasioamini alikuwa anataka watu wa Mungu wawe na uhuru wa kumtumikia Mungu kwa ukamilifu, kujiwekea mipaka ya utakatifu, kuwa na amani ya moyo, kukua kwa haraka kiroho na kuepusha mivutano isiyo na ulazima, na zaidi sana kuruhusu uwepo wa Mungu katika maisha yetu, haya ni maswala ya msingi sana kama tulivyojifunza ya kuwa kuna madhara ya kufungiwa nira na wasioamini, Lakini kuna faida kubwa za kutokufungiwa nira na wasioamini. Moja ikiwa pamoja na kufurahia uwepo wa Mungu hususani katika ndoa zetu, urafiki wa karibu, ushirika wa kibiashara na ufikiaji wa malengi ya kiungu.

1Wakorintho 7:35 “Nasema hayo niwafaidie, si kwamba niwategee tanzi, bali kwa ajili ya vile vipendezavyo, tena mpate kumhudumia Bwana pasipo kuvutwa na mambo mengine.”

Kuoa au kuolewa au kufanya agano na kuwa na ushirika wa karibu au kupatana yaani kufungiwa nira kwa kuwa na mahusiano ya karibu na mtu asiyemjua Mungu au kupata mafundisho ya kutosha kuhusu huduma ya Mungu kunatengeneza mazingira ya mgawanyiko na migogoro inayoathiri utumishi wako kwa Mungu, muelekeo wako kwa Mungu unaathiriwa na mtu asiyemjua Mungu, kama mtu anataka kumtumikia Mungu kwa uhuru ni vema ukajitoa katika nira hiyo na kama umeshaingia ni ngumu kujitoa utalibeba, lakini kama hujaingia chukua tahadhari za kibiblia

2Wakorintho 6:17-18 “Kwa hiyo, Tokeni kati yao, Mkatengwe nao, asema Bwana, Msiguse kitu kilicho kichafu, Nami nitawakaribisha.Nitakuwa Baba kwenu, Nanyi mtakuwa kwangu wanangu wa kiume na wa kike,”

Kanisa limeitwa au lina wito wa kuishi maisha matakatifu, maandiko yanakiri kwamba pasipo utakatifu haiwezekani kumuona Mungu, maisha ya Utakatifu yanahusisha kutengwa na kujitenga, Kwamba Mungu anakutenga wewe na mimi kwa kazi maalumu, sisi nasi tunawajibu wa kujitenga na dunia kwa sababu Mungu aliyetuita ni Mtakatifu kwa hiyo wito wa kutokufungiwa nira na wasioamini unamuita kila mmoja wetu kuishi maisha Matakatifu.

1Petro 1:15-16 “bali kama yeye aliyewaita alivyo mtakatifu, ninyi nanyi iweni watakatifu katika mwenendo wenu wote; kwa maana imeandikwa, Mtakuwa watakatifu kwa kuwa mimi ni mtakatifu.”

Waebrania 12:14Tafuteni kwa bidii kuwa na amani na watu wote, na huo utakatifu, ambao hapana mtu atakayemwona Bwana asipokuwa nao;”

Kufukia malengo ya kiroho kwa Amani – Kimsingi watu wanapokuwa wamefungiwa nira maana yake wanatengeneza mwelekeo mmoja na kwa sababu hiyo lengo lao la kimwili na kiroho linakuwa moja kwa msingi huo inakuwa rahisi kwao kutimiza makusudi yao kwa Amani na utulivu na hivyo lengo lao linakuwa rahisi na lenye kuzaa matunda, sawa na ng’ombe ambao wamefunzwa kulima maana yake wote wataifanya kazi ya kulima au kusukuma mkokoteni wa kizigo kwa ufanisi kwa sababu wote wana mafunzo yanayolingana, lakini wanyama kazi hao wanapokuwa hawana ulinganifu mambo huharibika mwenendo hauwezi kuwa sawa na kunatokea maumivu makali, kuumizana na kukwazana na kusababisha kutokufikiwa kwa malengo yanayokusudiwa, Nilielezewa na Marabi wa Kiyahudi kuhusu habari za Iditi  “Idit”  kwa mujibu wa maelezo yao katika vitabu vya masimulizi ya kiyahudi kiitwacho Midrash Aggadah, Idit lilikuwa jina la mke wa Lutu, Biblia hailelezi mengi kuhusu mke wa Lutu na wala haitaji jina lake, Lakini Marabi wa kiyahudi wanaeleza ya kuwa mwanamke huyu hakuwa mkarimu kwa wageni tofauti na ilivyokuwa na mumewe, Marabi wanasema mwanamke huyu alikuwa na tabia sawa na watu wengi walioishi Sodoma, ni wazi kuwa huenda Lutu alimpata mwanamke huyu katika miji hii, Mwanamke huyu hakuwa mwema na inaelezwa kuwa hata malaika wale wagani walipowatembelea ni Mumewe ndiye aliyeonekana kuwachangamkia, mke wa Lutu yaani Idit alitoka nje na kweneda kuomba chumvi kwa wanawake wa Sodoma, sio kuwa hakuwa na chumvi nyumbani kwake lakini alikuwa anataka watu wa mji ule wajue kuwa nymkbani kwake kuna wageni na kuwa aliandaa chumvi ya kuwatosha wao tu lakini kwa kuwa wamekuja wageni aliamua kutoka kuomba chumvi, kwa kusudi la kuwasengneya wageni na mumewe kuwa amepokea wageni, hata pamoja na ukarimu wa malaika ambao walimuokoa nayeye na kuwaonya wasitazame nyuma yeye aligeuka nyuma na akahukumiwa kuwa nguzo ya chumvi, hii ndio sababu iliyopelekea yeye kuachwa, Tabia ya mke wa Lutu inaweza kuonekana katika nyumba nyingi leo ambapo mwanaume anaweza kuwa mkarimu lakini mkewe akawa mchoyo au mwanamke anaweza kuwa mkarimu na mcheshi lakini mumewe akawa tofauti, mkali na hacheki na yeyote, wakati kanisa litakaponyakuliwa watu wengi wataachwa katika mtindo kama huu mmoja atwaliwa mmoja aachwa hii ni kwa sababu ya watu wengi kufungiwa nira katika ndoa moja na asiyeamini, au mtu mwenye tabia mbaya, kwa hiyo swala la kuhukumiwa kwa mke wa Lutu haikuwa swala la kugeuka nyuma pekee, lakini alikuwa ni mtu mwenye kudharau maagizo ya Mungu na kuyapuuzia wakati mumewe na watoto walikuwa waelekevu waliotii walichofundishwa

Mwanzo 19:25-26 “Akaangusha miji hiyo na Bonde lote, na wote waliokaa katika miji hiyo, na yote yaliyomea katika nchi ile. Lakini mkewe Lutu akatazama nyuma yake, akawa nguzi ya chumvi

Ni mpango wa Mungu kutuokoa wote pamoja na familia zetu, lakini tunapofunguwa nira na wasioamini tunaweza kujiletea maumivu sisi wenyewe, nadhani mojawapo ya maumivu yaliyomkuta Lutu sio kupoteza kila kitu lakini alimpoteza me wake mpendwa ambaye alimvumilia ijapo kuwa alikuwa na tabia mbaya ambazo malaika hawakuzivumilia, Malengo ya kuokolewa kwa familia yake hayakuweza kutimia.

Kupoteza furaha na utulivu wa kifamilia. – Pamoja na Baraka zote walizokuwa nazo Isaka na Rebeka tunataarifiwa katika maandiko kuwa maisha yao yalitiwa uchungu na kuhuzunishwa sana na wake wa Esau, Esau wakato wote alionyesha kuvutiwa sana na maswala ya dunia kuliko mambo ya Mungu kwa hiyo bila kujali wala kuchukua ushauri wa wazazi alioa wanawake wawili wa Kihiti, hawa walikuwa waabudu miungu, kwa sababu hiyo moyo wa Isaka na rebeka haukuweza kufurahia na wanawake hao pia waliondoa utulivu wa kifamilia katika maisha yao

Mwanzo 26:34-35 “Esau alipokuwa mwenye miaka arobaini, akamwoa Yudith, binti Beeri, mhiti na Basemathi, binti Eloni Mhiti, Roho zao Isaka na rebeka zikajaa uchungu kwaajili yao

Isaka na Rebeka walikumbuka jinsi Mungu alivyohusika katika upatikanaji wa mke wa Isaka Abrahamu alimuagiza mtumishi wake na mtumishi huyu aliomba na kuweka nadhiri, Mungu alihusika moja kwa moja katika upatikanaji wa Rebeka lakini sio ilivyokuwa kwa kijana wao yeye alijiolea tu sijui kama Isaka na Rebeka walihudhuria harusi hii, lakini ilitengeneza mgogoro na kuondoa furaha na utulivu wa kifamilia Biblia ya kiingereza inasema “Esau marriages with unbeliever wives made life bitter for Isaac and Rebekah” Isaka na Rebeka hawakuwa wabaguzi wa rangi, wala hawakuwa na nia ya kumkataza Esau kuoa mke zaidi ya mmoja kwa sababu yakobo pia alioa zaidi, lakini changamoto hapa ilikuwa tamaduni tofauti, na wakaanani walikuwa waovu na wasiomcha Mungu hivyo swala la kiroho kwao ndilo lilipewa kipaumbele

Kuweka usalama wa maisha ya kiroho – Watu wa Mungu wanapoharibu nira yao na Mungu na kujiunga na wale wasiompenda Mungu kimsingi wanaharibu usalama wao na kwa sababu hiyo wanakaribisha mashambulizi makubwa ya aina mbalimbali katika maisha yao ya kiroho, hakuna jambo tunaloweza kulifanya ili tumpendeze Mungu kila kitu kwa Mungu tunakipata kwa neema ya Mungu lakini hata hivyo naada ya kuokolewa neno la Mungu linatutaka tutembee katika utii wetu kwa Mungu ili adui aweze kutukimbia, Mungu kamwe hawezi kuubariki uhusiano ambao unakwenda kinyume na mapenzi yake, kufungiwa nira na wasioamini kunatunyima watu wa Mungu kuzifikia usalama unaokusudiwa na Mungu kwa sababu upande mmoja utakuwa unaharibu na upande mwingine utakuwa unajaribu kutengeneza, ulinzi wa kiungu unaharibiwa pale mtu wa Mungu anapojiungamanisha na mahusiano ambayo kimsingi ni machukizo kwa Mungu

Yeremia 5:3-6 “Ee Bwana, macho yako je! Hayaangalii uaminifu? Umewapiga, lakini hawakuhuzunika; umewakomesha, lakini wamekataa kurudiwa wamefanya nyuso zao kuwa ngumu kuliko mwamba wamekataa kurudi. Ndipo nikasema, Hakika, hawa ni maskini; ni wajinga hawa; maana hawaijui njia ya Bwana, wala hukumu ya Mungu wao; nitawaendea watu wakubwa, nami nitasema nao; kwa maana hao wanaijua njia ya Bwana, na hukumu ya Mungu wao. Bali hawa kwa nia moja wameivunja nira, na kuvikata vifungo. Basi, kwa hiyo, simba atokaye mwituni atawaua, mbwa-mwitu wa jioni atawateka, chui ataivizia miji yao, kila mtu atokaye humo atararuliwa vipande vipande; kwa sababu makosa yao ni mengi, na kurudi nyuma kwao kumezidi.”         

Kwaajili ya kuepusha migogoro na migongano – Mkristo kuoa au kuolewa na mtu asiyeamini ni nira inayoweza kusababisha migongano ya kiimani, kiibada, kimaadili na kimaamuzi katika familia, Aidha kushirikiana kibiashara na mtu asiyeamini kunaweza kuleta maamuzi yanayopingana na kanuni za kiroho, rushwa, wizi,  udanganyifu, tamaa, kujitafutia na ushawishi wa tabia mbaya, Ushirika wa kiroho au kujiunga ma makundi yenye mafundisho potofu ni hatari kwa mustakabali wa kiimani ni kwaajili ya haya Neno la Mungu linatuagiza kuacha kufungiwa nira na wasioamini, aidha ukiacha ukweli kuwa ni hatari kwa imani, inaharibu baraka za Mungu, inaharibu hatima ya mtu, inaharibu uhuru wa mtu kuabudu na kumtumikia Mungu inaathiri uwepo wa Mungu na uhusiano wetu, Nira na wanaoamini inakuhakikishia usafi wa kiibada na kiimani na usalama, Kujifungia nira na wasioamini kunatuletea uchafu wa kiroho na kiimani kwa hiyo ni muhimu kujiepusha na ndoa za kisheria na wasioamini, kujiepusha na mikataba au mapatano yatakayokulazimu kufanya dhambi, kujiepusha na kumuwekea dhamana mtu ambaye haamini asije akakuliza na kukuweka matatani, ili uwe safi chagua marafiki na watu wa karibu ambao wanakuleta karibu na Mungu na sio vinginevyo, chagua watu ambao mna kusudi moja lenye kuwiana na ufalme wa Mungu.

Kumbuka kuwa fundisho hili halihusiani na kujiepusha kabisa na watu wa dunia hii, kwani kwa sehemu sisi ni sehemu ya jamii, lakini fundisho hili lina mkazo katika watu tunaowaleta karibu, wenye ushawishi, kikazi, kimkataba, kiagano, kiimani, kindoa na urafiki, hao ni lazima wawe watu wa Imani moja na wewe na wengine tunaishi nao katika hali ya kawaida kwa sababu ingelitulazimu kuhama ulimwenguni

Yohana 17:14-16 “Mimi nimewapa neno lako; na ulimwengu umewachukia; kwa kuwa wao si wa ulimwengu, kama mimi nisivyo wa ulimwengu. Mimi siombi kwamba uwatoe katika ulimwengu; bali uwalinde na yule mwovu.Wao si wa ulimwengu, kama mimi nisivyo wa ulimwengu.”

Hitimisho:

Mji wa Korintho ulikuwa ni kitovu kikubwa sana cha utamaduni wa Kigiriki, Uchumi na ibada za kipagani, sawa tu na dunia tuliyo nay oleo, na Wakristo wa Korintho walikuwa wameokolewa kutoka katika mazingira ya kuabudiwa kwa miungu mingi kama Aphrodite na zeuz, tamaduni mchanganyiko na biashara lakini pia ulikuwa mji mchafu kingono na ndoa zisizokuwa na uadilifu, mahusiano ya kijamii yalikuwa na machanganyiko wa kitamaduni ambazo kimsingi haikuwa zinajali lolote kuhusu Mungu, Kwaajili ya kuwalinda watu hususani Wakristo ili wasirudi nyuma. Paulo anakataza waamini kujiungamanisha katika fungano la ukaribu sana na watu wa Dunia ile, Paulo alikuwa akionyesha wazi kuwa watu waliookolewa wana nguvu tofauti, hatua tofauti, mwenendo tofauti, hisia tofauti, malengo tofauti na mazigo tofauti kwa hiyo Paulo anatumia fundisho lile lile la kiyahudi katika Torati akiwataka wakorintho wasijunganishe katika uhusiano wa karibu na amaagano na ushirika wa maisha na urafiki na watu waovu baada ya wao kuokolewa, huu ulikuwa ni wito wa kuishi maisha matakatifu lakini pia wa kujilinda kwa mujibu wa tamaduni na maisha ya Ukristo, Paulo alitaka watu wakuze uhusiano wao na Kristo maana yake kujitoa katika nira ya Kristo kwa hiyo wakristo wanaonywa kuhusu ndoa, biashara na urafiki wa karibu  na watu wanaoweza kuleta ushawishi wa uharibifu wa uadilifu katika maisha yao hii itaweka sawa ushirika wa kimaadili, kutiana moyo katika ukuaji wa kiroho, Kuimarisha na kuifanya kazi ya Mungu kwa Amani na Kukaribisha uwepo wa Mungu na Baraka zake katika maisha yake kwa hiyo ingawa wito huu u naonekana kuwa mkali lakini ni wenye manufaa makubwa kwa mustakabali wa furaha ya kweli katika maisha ya Ukristo;

 

Mathayo 11:28-29 “Njoni kwangu,ninyo nyote msumbukao na wenye kuelemewa na mizigo nami nitawapumzisha.Jitieni nira yangu mjifunze kwangu; kwa kuwa mimi ni mpole na mnyenyekevu wa moyo nanyi mtapata raha nafsini mwenu; kwa maana nira yangu ni laini na Mzigo wangu ni mwepesi.”    

Na Rev. Innocent Samuel Kamote

Mkuu wa wajenzi mwenye Hekima