Jumamosi, 27 Desemba 2025

Kupata na kujuta!

 


1Timotheo 6:6-10 “Walakini utauwa pamoja na kuridhika ni faida kubwa. Kwa maana hatukuja na kitu duniani, tena hatuwezi kutoka na kitu; ila tukiwa na chakula na nguo tutaridhika na vitu hivyo. Lakini hao watakao kuwa na mali huanguka katika majaribu na tanzi, na tamaa nyingi zisizo na maana, zenye kudhuru, ziwatosazo wanadamu katika upotevu na uharibifu. Maana shina moja la mabaya ya kila namna ni kupenda fedha; ambayo wengine hali wakiitamani hiyo wamefarakana na Imani, na kujichoma kwa maumivu mengi.”




Utangulizi

Bila shaka umewahi kushuhudia katika maisha haya kama mwanadamu kuwa unaweza kuwa na hamu au shauku ya kupata kitu fulani na ukapambana mpaka ukakipata na baada ya kuwa umekipata ukaanza kujuta moyoni, Hali hii inaweza ikatokea mara baada ya kufanya maamuzi kadhaa katika maisha yetu kisha baada ya maamuzi hayo unasikia hisia za majuto, unajiona kama umefanya maamuzi duni, ya kijinga na kipumbavu au kama umefanya makosa ya kiufundi umekosea malengo, au hujafanya maamuzi sahihi, wakati mwingine maamuzi ya aina hiyo yanaweza kuleta uchungu na hisia hasi na kuathiri afya na maendeleo ya mtu, kimwili, kiroho na kisaikolojia, ingawa kujuta pia kunaweza kujenga hisia chanya na kumfanya mtu kufanya maamuzi mazuri baadaye, maa na yake ni nini?, si kila kitu tunachikitaka na kufanikiwa kukipata duniani kinaweza kutuletea furaha, viko vitu vingine tunaweza tukavitamani sana lakini baada ya kuvipata vinaweza kuwa chanzo cha maumivu makubwa na huzuni na majuto, vitu hivyo inaweza kuwa mali, fedha, vyeo, mahusiano na kadhalika ambavyo tumevipigania kuvipata kwa shauku/tamaa lakini baadaye vinatuletea maumivu.

Yakobo 4:3 “Vita vyatoka wapi, na mapigano yaliyoko kati yenu yatoka wapi? Si humu, katika tamaa zenu zifanyazo vita katika viungo vyenu? Mwatamani, wala hamna kitu, mwaua na kuona wivu, wala hamwezi kupata. Mwafanya vita na kupigana, wala hamna kitu kwa kuwa hamwombi! Hata mwaomba, wala hampati kwa sababu mwaomba vibaya, ili mvitumie kwa tamaa zenu. Enyi wazinzi, hamjui ya kwamba kuwa rafiki wa dunia ni kuwa adui wa Mungu? Basi kila atakaye kuwa rafiki wa dunia hujifanya kuwa adui wa Mungu.”

Watu wengi sana duniani wametamani sana kupata mali, vyeo, na hata mahusiano Fulani kwa tamaa zao, lakini baadaye walijuta na kulia machozi, ni muhimu sana kupata lolote tunalolitamani katika mapenzi ya Mungu na sio kwa tamaa ya kibinadamu, sio kila kitu tunachokitaka duniani kinaweza kutupa raha, na furaha, vingine vinaweza kutuletea maumivu, uchungu na majuto, mengi, wengi wamejilaumu wenyewe, kujikosoa na kujisikia vibaya au kukata tamaa kwa sababu ya hali hii “Getting and regretting” yaani kupata na kujuta kisaikolojia tendo hili linaitwa “Cognitive dissonance” ambalo ni tendo la kukosa raha, baada ya mambo kwenda kinyume na ulivyoamini!

Leo kwa msingi huo tutachukua muda kujifunza somo hili Kupata na kujuta kwa kuzingatia vipengele vitatu vifuatavyo;-

·         Maana ya kupata na kujuta

·         Kupata na kujuta.

·         Jinsi ya kupata katika mpango wa Mungu


Maana ya kupata na kujuta

Kupata na kujuta ni tendo la kupata huzuni, kukata tamaa, kupata masononeko katika akili yanayokuja baada ya kupata jambo fulani ambalo ulitarajia kuwa litakupa furaha lakini ukajutia kuwa haikuwa kama ulivyokuwa unafikiri, na ukatamani kama ungelifanya vinginevyo, hii ni mojawapo ya sehemu ya kawaida katika maisha ambayo imewakumba watu wengi, aidha baada ya kupata nafasi fulani nzuri na kushindwa kuitumia au kupata nafasi fulani wakaitumia lakini isilete furaha au matarajio uliyoyafikiri, tendo hilo kisaokolojia linaitwa Cognitive dissonance – Psychological conflict resulting from incongruous beliefs and attitudes held simultaneously, kwa Kiswahili tunaweza kusema Majuto ni Matokeo ya mgogoro wa kisaikolojia unaotokana na kutokuenda sawa kwa kile ulichikiamini au kukitarajia sawa na mtazamo ulioufikiria, Kwa Kiebrania linatumika neno “Nâcham” naw- kham kimatamshi,  kwa kiingereza to sigh – physical and emotional response to strong feeling like grief, regret, repent Kwa mfano Mungu alipomuumba mwanadamu, aliatarajia wanadamu wataishi kwa shukurani na utii kwa Mungu, lakini badala yake  wanadamu wakaanza kuishi tofauti na kile Mungu alichokuwa amekitarajia kwa hiyo Mungu alijuta, aidha Mungu alijuta pia alipomtawaza Sauli akijua kuwa atatii yote anayomwagiza, lakini Sauli alirudi nyuma asifuate aliyoagizwa na Mungu

Mwanzo 6: 1-6 “Ikawa wanadamu walipoanza kuzidi usoni pa nchi na wana wa kike walizaliwa kwao, wana wa Mungu waliwaona hao binti za wanadamu ya kuwa ni wazuri; wakajitwalia wake wo wote waliowachagua. BWANA akasema, Roho yangu haitashindana na mwanadamu milele, kwa kuwa yeye naye ni nyama; basi siku zake zitakuwa miaka mia na ishirini. Nao Wanefili walikuwako duniani siku zile; tena, baada ya hayo, wana wa Mungu walipoingia kwa binti za binadamu, wakazaa nao wana; hao ndiyo waliokuwa watu hodari zamani, watu wenye sifa. BWANA akaona ya kuwa maovu ya mwanadamu ni makubwa duniani na kwamba kila kusudi analowaza moyoni mwake ni baya tu sikuzote. BWANA akaghairi kwa kuwa amemfanya mwanadamu duniani, akahuzunika moyo.”

1Samuel 15:10-11 “Ndipo neno la Bwana likamjia Samweli, kusema, Najuta kwa sababu nimemtawaza Sauli awe mfalme; maana amerudi nyuma, asinifuate, wala hakufanya nilivyomwamuru. Samweli akasikitika, akamlilia Bwana usiku kucha.”                

Katika maandiko yote hayo lugha ya kiebrania inayotumika ni “Nâcham” ikimaanisha kuwa Mungu alijuta baada ya kuwa alifanya jambo kwa nia njema lakini baadaye hakupata matokeo kama yale aliyokuwa ameyaamini au kuyategemea au kuyatarajia huu ni mfano sasa wa kupata na kujuta, Katika maisha, kupata na kujuta kumewatokea watu wengi sana na kunaendelea kuwatokea, Bwana ampe neema kila mmoja wetu asitembee katika maisha ya majuto na badala yake aweze kufurahia maisha, Mungu akupe akili hizo na ufahamu huo, isitokee ukaja kujuta katika maisha yako Ameeeeen

Kupata na kujuta.

Kila mwanadamu anapaswa kuwa makini sana katika maeneo yote ya maamuzi katika maisha yake kwani kanuni inayotumika hapo ndiyo ambayo inaweza kutuletea furaha au majuto, endapo maamuzi yetu yatafanyika yakiwa yanaongozwa na tamaa na misukumo ya kibinadamu bila kuzingatia ua kufikiri sana katika upana wake kwa njia za kiungu na kutimiza mapenzi ya Mungu tunaweza kujikuta tunaingia katika kundi la watu wanaojuta katika maisha yao, Neno llinatuasa:-

Mithali 3:5-7 “Mtumaini Bwana kwa moyo wako wote, Wala usizitegemee akili zako mwenyewe; Katika njia zako zote mkiri yeye, Naye atayanyosha mapito yako. Usiwe mwenye hekima machoni pako; Mche Bwana, ukajiepushe na uovu.”   

Maandiko yanaonyesha kuwa wako watu wengi sana ambao walitazama kitu kwa mitazamo yao na kukitamani lakini bila kuzingatia mapenzi ya Mungu na wakapata lakini walijuta sana baadaye

-          Hawa – Mwanzo 3:6-7 “Mwanamke alipoona ya kuwa ule mti wafaa kwa chakula, wapendeza macho, nao ni mti wa kutamanika kwa maarifa, basi alitwaa katika matunda yake akala, akampa na mumewe, naye akala. Wakafumbuliwa macho wote wawili wakajijua kuwa wa uchi, wakashona majani ya mtini, wakajifanyia nguo.”

 

Adamu na Hawa walijutia sana katika maisha yao na vizazi vyao swala zima la kutokumtii Mungu na kufuata mapenzi yao kwa kula mti waliokatazwa na Mungu, wao waliutamani ule mti na katika fikira zao walifikiri wanaweza kupata furaha wakala kwa tamaa ya kufanana na Mungu, na kwa masikitiko makubwa wakagundua kuwa wameingia matatizoni na wamekuwa uchi kabisa, uamuzi wao uliwapa kujuta siku zote za maisha yao kupata na kujuta

 

-          Lutu – alifanya uamuzi wa kuchagua kuishi katika bonde la Sodoma ambalo kwa macho ya kawaida liloonekana kuwa kama bonde la Mungu, ardhi ilikuwa nzuri yenye kuvutia na akaamua kuishi huko nadhani pia alioa huko, alipata lakini alitoka na majuto kwani alipoteza kila kitu alichokuwa nacho na hata mkewe pia na kujikuta akiishi katika pango akiwa masikini na asiyekuwa na kitu, na kuishia katika uvunjifu mkubwa wa kimaadili uliochagiwa bintize.

 

Mwanzo 13:10-13 “Lutu akainua macho yake, akaliona Bonde lote la Yordani, ya kwamba lote pia lina maji, kabla BWANA hajaharibu Sodoma na Gomora, lilikuwa kama bustani ya BWANA, kama nchi ya Misri hapo unapokwenda Soari. Basi Lutu akajichagulia Bonde lote la Yordani; Lutu akasafiri kwenda upande wa mashariki; wakatengana wao kwa wao. Abramu akakaa katika nchi ya Kanaani, na Lutu akakaa katika miji ya lile Bonde; akajongeza hema yake mpaka Sodoma.Lakini watu wa Sodoma walikuwa wabaya, wenye kufanya dhambi nyingi sana juu ya BWANA.”

 

Mwanzo 19:26-30 “Lakini mkewe Lutu akatazama nyuma yake, akawa nguzo ya chumvi. Ibrahimu akatoka asubuhi kwenda mahali aliposimama mbele za BWANA, naye akatazama upande wa Sodoma na Gomora na nchi yote ya hilo Bonde, akaona, na tazama, moshi wa nchi ukapanda, kama moshi wa tanuru. Ikawa Mungu alipoiharibu miji ya Bondeni, Mungu akamkumbuka Ibrahimu, akamtoa Lutu katika maangamizi alipoiangamiza miji hiyo aliyokaa Lutu.Lutu akapanda kutoka Soari akakaa mlimani, na binti zake wawili pamoja naye, kwa sababu aliogopa kukaa katika Soari. Akakaa katika pango, yeye na binti zake wawili.”

 

-          Amnoni mwana wa Daudi alimpenda sana Tamari binti ya baba yake alimpenda sana mpaka akawa anakonda na kuumwa, alimtamani sana alimpenda mno ndio maandiko yanavyotueleza mpaka akapanga mikakati ya kumpata kwa hila, hata hivyo baada ya kumpata tu neno la Mungu linasema alimchukia machukio makuu sana kuliko yale mapenzi aliyokuwa amempenda kwanza jambo hili lilimfanya apate lakini ajute

 

2Samuel 13:11-19 “Naye alipokwisha kuileta karibu naye, ili ale, Amnoni akamkamata, akamwambia, Njoo ulale nami, ndugu yangu. Naye akamjibu, La, sivyo, ndugu yangu, usinitenze nguvu; kwani haifai kutendeka hivi katika Israeli; usitende upumbavu huu. Nami nichukue wapi aibu yangu? Wewe nawe utakuwa kama mmoja wa wapumbavu wa Israeli. Basi, sasa, nakusihi, useme na mfalme; kwa maana hatakukataza kunioa. Walakini yeye hakukubali kusikiliza sauti yake; naye akiwa na nguvu kuliko yeye, akamtenza nguvu, akalala naye. Kisha Amnoni akamchukia machukio makuu sana; kwa kuwa machukio aliyomchukia yakawa makuu kuliko yale mapenzi aliyokuwa amempenda kwanza. Amnoni akamwambia, Ondoka, nenda zako. Naye akamwambia, Sivyo, kwa kuwa mabaya haya ya kunitoa ni makuu kuliko yale uliyonitendea. Lakini alikataa kumsikiliza. Ndipo akamwita mtumishi wake aliyemtumikia, akasema, Mtoe sasa mwanamke huyu kwangu, ukafunge mlango nyuma yake. Naye alikuwa amevaa kanzu ndefu; kwa kuwa kwa nguo hizo huvikwa binti za mfalme waliokuwa wanawali. Ndipo mtumishi wake akamleta nje, akafunga mlango nyuma yake. Naye Tamari akatia majivu kichwani mwake, akairarua hiyo kanzu ndefu yake aliyoivaa, akaweka mkono kichwani akaenda zake huku akilia kwa sauti.”

 

 

-          Yuda Iskariote – alitamani sana fedha, alifahamu au kudhani ya kuwa anaweza kumsaliti Yesu Kwa vipande 30 vya fedha, akidhani kuwa labda Yesu angeliponyoka katika mikono ya adui zake, hakufikiri kwa kina zaidi ya tamaa zake lakini baadaye alijutia sana umauzi wake alizitupa fedha hizo na kwenda kujinyonga, kupata fedha sio kubaya lakini kutafuta fedha nje ya mapenzi ya Mungu au kufanya mambo kwa tamaa ni jambo baya sana linaloweza kutuletea majuto, Kwa hiyo Yusa alifanikuwa kupata fedha kwa kumsaliti yetu Lakini alijutia

 

Mathayo 26:14-16 “Wakati huo mmoja wa wale Thenashara, jina lake Yuda Iskariote, aliwaendea wakuu wa makuhani, akasema, Ni nini mtakachonipa, nami nitamsaliti kwenu? Wakampimia vipande thelathini vya fedha. Tokea wakati huo akawa akitafuta nafasi apate kumsaliti.”

               

Mathayo 27:1-5 “Na ilipokuwa asubuhi, wakuu wa makuhani wote na wazee wa watu wakafanya shauri juu ya Yesu, wapate kumwua; wakamfunga, wakamchukua, wakampeleka kwa Pilato aliyekuwa liwali. Kisha Yuda, yule mwenye kumsaliti, alipoona ya kuwa amekwisha kuhukumiwa, alijuta, akawarudishia wakuu wa makuhani na wazee vile vipande thelathini vya fedha, akasema, Nalikosa nilipoisaliti damu isiyo na hatia. Wakasema, Basi, haya yatupasani sisi? Yaangalie haya wewe mwenyewe. Akavitupa vile vipande vya fedha katika hekalu, akaondoka; akaenda, akajinyonga.”

Kusudi la Mungu ni kumtunza mwanadamu na maumivu mengi, kumlinda mwanadamu dhidi ya tamaa, kumkumbusha mwanadamu ya kuwa anapaswa sana kumtegemea Mungu katika maamuzi yake yote na njia zake zote, wanadamu wengi sana waliookoka na wale wasiookoka wamejikuta katika madhara makubwa kwa sababu ya kuongozwa na tamaa na matakwa yao wenyewe, ni vema kila unapofika wakati wa kufanya maamuzi watu wakawa wanautafuta uso wa Mungu kwa bidii ili kuyapata mapenzi ya Mungu badala ya kuzifuata njia zetu wenyewe ambazo baadaye zinaweza kutuletea majuto, Neno la Mungu linayo maelekezo ya kutosha ya namna ya kupata yale tuyatakayo katika mapenzi ya Mungu na ikiwa hivyo katika maisha yetu tutaepuka kwa kiwango kikubwa kujuta.

Mithali 14:12-14 “Iko njia ionekanayo kuwa sawa machoni pa mtu, Lakini mwisho wake ni njia za mauti. Hata wakati wa kucheka moyo huwa na huzuni; Na mwisho wa furaha ni uzito wa moyo. Ageukaye moyoni hushiba njia zake mwenyewe; Na mtu mwema ataridhika nafsini mwake.”

Jinsi ya kupata katika mpango wa Mungu

Maisha yamejaa majuto mengi sana wako watu wanajuta kwa sababu mbalimbali katika maisha walipata lakini wanajuta, ukifanya utafiti, wako watu wamechoka mno mioyo yao imejaa simamzi na uchungu kwa sababu walipata au walifanya jitihada za kupata lakini wanajuta kwa namna moja ama nyingine, yale waliyoyapigania ili wapate yalileta majuto badala ya furaha, yale yaliowapotezea muda mwingi sana wakawekeza huko yakawalipa mabaya wasiotarajia, sasa wanajuta, wako wanaojuta kwa sababu, Walipopata kazi, walifanya kazi kwa bidii na kwa kujituma sana lakini hawakutoa muda wa kutosha kwa familia zao, marafiki zao na ndugu na jamaa, wakati wote walikuwa bize na kazi zao lakini walipojikuta wako vitandani na wanakaribia kufa walijuta kwa sababu kazi walizipata  na fedha walizipata lakini walijikuta wanafanya kazi sana na kutumia masaa mengi makazini na wakakosa wakati muhimu wa kuwa na familia zao, nahata kuwaweka sawa watoto wao, wanakuja kubaini watoto wamepotoka, wamekuwa bila upendo wa baba na mama,

Wako waliokataa wachumba zao kwa sababu walichelewa kuwaoa kwa sababu ya umasikini, nitamsubiria mpaka lini, mtu akaamua kuolewa na kijana aliyejitokeza kwa sababu ana kazi nzuri na gari nzuri, na pesa bila kujiuliza alivipataje lakini baada ya maisha kuendelea maisha yalitoa majibu tofauti, walipoteza upendo wa dhati kwa sababu ya vitu vinavyoonekana kwa muda sasa wanajuta

Wako watu ambao hawakuishi maisha yao halisi, na badala yake waliishi maisha ya kuigiza, wakitaka kuwafurahisha wengine walifurahia kusifiwa na kutambuliwa na watu, hawakuchagua ndoto zao walichagua ndoto za wazazi wao, hawakuchagua waume au wake waliowapenda wakachagua wale waliopendekezwa kwao na wachungaji, mabosi wao na vinginevyo, hawakuchagua kazi zao na fani zao walichagua kile dunia inakitaka kwaajili yao na wakawekeza muda wao huko na sasa wanajuta

Wako watu ambao wanajuta kwa sababu hawakuwa na muda wa kutunza afya zao, waliishi maisha ya hovyo, mabaya, hawakuwa na muda wa kutengeneza na watu, waliharibu mahusiano, na watu, familia zao na kupuuzia mapatano, na sasa wanajuta, wako waliopuuzia  muda wa kulala, muda wa kufanya mazoezi, walikunywa misoda na mavitu ya Super-market na sasa wanagundua kuwa wameharibu kila kitu wana huzuni kwa sababu hawakufanya mazoezi, wana huzuni kwa sababu hawakuzingatia lishe bora, wana huzuni, kwa sababu hawakufanya mapatano, wana huzuni kwa sababu hawakuwa wanalala usingizi wa kutosha afya zimeharibika na sasa wanajuta, wako hata waliokuwa wakifunga kwa kusudi la kuutafuta uso wa Bwana lakini walifunga hovyo hovyo bila kuzingatia kanuni za afya na sasa wana madonda ya tumbo, na hawawezi kufunga tena na wanajuta

Wako watu ambao wanajuta kwa sababu hawakuwekeza, hawakuweka akiba za kutosha hawakufikiri mambo ya baadaye sasa ni masikini, hawana fedha, hawakuwekeza mashamba wala mifugo hawakujali tabia zao zitawaletea matunda gani ya baadaye na sasa wanajuta, hawakupanga wanazaa watoto wangapi na kwa kiasi gani, wao kila kilichotokea kiliwatokea kama bahati tu, wako wanaojuta kwa usaliti, kupigania vyeo wakavipata lakini baadaye wakajuta hata kwanini walipigania vyeo hivyo, kutaka umaarufu, kuoa au kuolewa na watu wasio sahihi na kadhalika na sasa wao wako Jehanamu ya moto wa ndoa zao wakati wengine wako Paradiso umepata lakini unajuta!, wako waliozalishwa wakiwa nyumbani, waliona raha kujirusha lakini sasa wanajuta, wako ambao wameolewa na kuachika, wako waliotoa talaka na wanajuta, wako waliodai talaka na sasa wanajuta  hii ndio hali halisi ya Dunia pale tunapofanya mambo na kuchagua mambo kwa kuyapa uthamani wa kwetu wenyewe machoni petu wenyewe na kufanya mambo ambayo yanaweza kutufurahisha kwa muda mfupi badala ya kuwaza yatakayotufurahisha kwa muda mrefu, chaguzi za namna hiyo ni chaguzi za kiesharati kwa mujibu wa maelekezo ya kimaandiko, mwesharati ni mtu anayewaza kumaliza haja zake za muda mfupi tu na ikamgharimu maisha yake, badala ya kufikiri mbele hii ilikuwa changamoto ya Esau ambaye alijuta sana baadaye baada ya kuuza urithi wake kwa sikumoja.

Waebrania 12:16-17 “Asiwepo mwasherati wala asiyemcha Mungu, kama Esau, aliyeuuza urithi wake wa mzaliwa wa kwanza kwa ajili ya chakula kimoja. Maana mwajua ya kuwa hata alipotaka baadaye kuirithi Baraka, alikataliwa (maana hakuona nafasi ya kutubu), ijapokuwa aliitafuta sana kwa machozi.”

Wewe hapo ulipo ulitamani nini na ukakitafuta na kukipigania kwa nguvu zako zote na ukakipata lakini sasa unajuta moyoni, wako watu wengi wenye majuto ya kila aina hapa duniani na wewe sio wa kwanza sisi kama wanadamu tunaweza kufanya maamuzi ambayo baadae yanaweza kutuletea majuto makubwa sana katika mioyo yetu! Tufanyeje tujiue, turudi nyuma hapana tunashauriwa cha kufanya Na maandiko  

Ufanyeje sasa ili usishi kwa majuto?

Mungu wakati mwingine anatutaka tuwe na subira, subira hupita njia ndefu na ngumu sana na ndio maana watu wengi hawaipendi njia hii, ni njia ngumu lakini inaweza kutuletea matokeo mazuri ya kiungu na kuiungwana unajua Mungu hufanya mambo kwa wakati, lakini mwanadamu hutaka matokeo ya haraka na ni vigumu kwetu kuvumilia na kusubiri wakati wa Mungu, kwa haraka zetu.

Muhubiri 3:11 “Kila kitu amekifanya kizuri kwa wakati wake; tena ameiweka hiyo milele ndani ya mioyo yao; ila kwa jinsi mwanadamu asivyoweza kuivumbua kazi ya Mungu anayoifanya, tangu mwanzo hata mwisho.”

Mungu anatutaka tutangulize faida za kiroho kabla ya zile faida za mwilini, wengi wanaopitia njia za majuto ni wale ambao tunafikiri kwa jinsi ya mwili, kwa kuangalia vinavyoonekana na kupuuzia vile visivyoonekana ambayo kwa asili ni vya milele na hutupa furaha ya kudumu, ni lazima tuutafute kwanza ufalme wa Mungu na haki yake na mengine yote tutazidishiwa

Luka 12:16-21 “Akawaambia mithali, akisema, Shamba la mtu mmoja tajiri lilikuwa limezaa sana; akaanza kuwaza moyoni mwake, akisema, Nifanyeje? Maana sina pa kuyaweka akiba mavuno yangu. Akasema, Nitafanya hivi; nitazivunja ghala zangu, nijenge nyingine kubwa zaidi, na humo nitaweka nafaka yangu yote na vitu vyangu. Kisha, nitajiambia, Ee nafsi yangu, una vitu vyema vingi ulivyojiwekea akiba kwa miaka mingi; pumzika basi, ule, unywe, ufurahi. Lakini Mungu akamwambia, Mpumbavu wewe, usiku huu wa leo wanataka roho yako! Na vitu ulivyojiwekea tayari vitakuwa vya nani? Ndivyo alivyo mtu ajiwekeaye nafsi yake akiba, asijitajirishe kwa Mungu.”

Nadhani kila unapofikia wakati wowote katika maisha mahali ambapo tunataka kufanya uamuzi basi ni vema sana tukatafuta sana mapenzi ya Mungu na uongozi wa Mungu neno linasema usizitegemee akili zako mwenyewe bali katika njia zako zote mtegemee Mungu

Warumi 8:13-16 “kwa maana kama tukiishi kwa kufuata mambo ya mwili, mwataka kufa; bali kama mkiyafisha matendo ya mwili kwa Roho, mtaishi. Kwa kuwa wote wanaoongozwa na Roho wa Mungu, hao ndio wana wa Mungu. Kwa kuwa hamkupokea tena roho wa utumwa iletayo hofu; bali mlipokea roho ya kufanywa wana, ambayo kwa hiyo twalia, Aba, yaani, Baba. Roho mwenyewe hushuhudia pamoja na roho zetu, ya kuwa sisi tu watoto wa Mungu;”

Mithali 3:5-7 “Mtumaini Bwana kwa moyo wako wote, Wala usizitegemee akili zako mwenyewe; Katika njia zako zote mkiri yeye, Naye atayanyosha mapito yako. Usiwe mwenye hekima machoni pako; Mche Bwana, ukajiepushe na uovu.”

Linda dhamiri yako wakati wote unapotaka jambo - unataka hicho unachokitaka kwa sababu gani? Mungu huangalia nia ya moyo na kuhukumu kulingana na nia ya moyo, kama kuna kitu unakihitaji lakini kwa tamaa unaweza usipewe au unaweza ukapewa lakini kikakutokea puani

Hesabu 11:18-20 “Kisha uwaambie watu hawa, Jitakaseni nafsi zenu kabla ya kesho, nanyi mtakula nyama; kwa maana mmelia masikioni mwa Bwana, mkisema, Ni nani atakayetupa nyama, tule? Maana huko Misri tulikuwa na uheri. Basi kwa sababu hiyo Bwana atawapa nyama, nanyi mtakula.Hamtakula siku moja, wala siku mbili, wala siku tano, wala siku kumi, wala siku ishirini; lakini mtakula muda wa mwezi mzima, hata hapo nyama hiyo itakapotoka katika mianzi ya pua zenu, nanyi mtaikinai, kwa sababu mmemkataa Bwana aliye kati yenu, na kulia mbele zake, mkisema, Tulitoka Misri kwa maana gani?

Hata kama tumemkosea Mungu na ikaleta majuto katika maisha yetu, ni Muhimu kwetu tukamrudia Mungu huyo huyo, kwa toba, kukiri, na kuutafuta uso wake tena, Upendo wa Mungu na rehema zake hauna mipaka, tukinyenyekea kwake atatupokea tena kama ilivyokuwa kwa mwana mpotevu, kupoteza kwetu sio mwisho wa maisha, kwani Baba wa rehema anayi nafasi nyingine, ttutafute uwepo wake naye atatutia nguvu na kuturejesha tena

Luka 15:17-20 “Alipozingatia moyoni mwake, alisema, Ni watumishi wangapi wa baba yangu wanaokula chakula na kusaza, na mimi hapa ninakufa kwa njaa. Nitaondoka, nitakwenda kwa baba yangu na kumwambia, Baba, nimekosa juu ya mbingu na mbele yako; sistahili kuitwa mwana wako tena; nifanye kama mmoja wa watumishi wako. Akaondoka, akaenda kwa babaye. Alipokuwa angali mbali, baba yake alimwona, akamwonea huruma, akaenda mbio akamwangukia shingoni, akambusu sana.”

Hitimisho:

Mpango wa kamili wa Mungu ni kila mmoja wetu kuyafurahia maisha, Mungu kama Baba aliye mwema anatufikiria mema na yuko kwaajili yetu, lakini pia yule muovu yuko, hata hivyo pamoja na kuweko kwa yule muovu, na majaribu mbalimbali mpango wa Mungu ni kuhakikisha ya kuwa anatubariki na kutupa mambo ya kudumu ambayo kimsingi hatachanganya nayo na huzuni wala majuto. Baraka za kweli kutoka kwa Mungu ni zile zinazokuja kwetu na hazituletei majuto, ukipata katika mpango wa Mungu bila ya hila, utaufurahia uwepo wa Mungu maisha yako yote, Bwana ampe neema kila mmoja wetu kuwa na Baraka za Mungu zisizo changamana na huzuni wala majuto. Amen

Mithali 10:22 “Baraka ya Bwana hutajirisha, Wala hachanganyi huzuni nayo.”

 

Na. Rev. Innocent Samuel Kamote

Mkuu wa wajenzi mwenye Hekima

Hakuna maoni: