2Wafalme 20:1-3 “Siku hizo Hezekia akaugua,
akawa katika hatari ya kufa. Isaya, nabii, mwana wa Amozi, akamjia akamwambia,
Bwana asema hivi, Tengeza mambo ya nyumba yako; maana utakufa, wala hutapona.
Basi Hezekia akajigeuza, akaelekeza uso wake ukutani, akamwomba Bwana akasema,
Nakusihi, Bwana, ukumbuke sasa, jinsi nilivyokwenda mbele zako katika kweli na
kwa moyo mkamilifu, na kutenda yaliyo mema machoni pako. Hezekia akalia sana
sana.”
Utangulizi:
Moja ya wafalme na watawala wa
ufalme wa Yuda aliyekuwa mwaminifu sana ni pamoja na Hezekia, Ni mfalme
aliyemcha Mungu na kufanya mapinduzi makubwa ya uamsho ikiwa ni pamoja na
kurejesha ibada ya Mungu wa kweli katika Hekalu lililokuwako Yerusalem na
kukomesha kabisa ibada za kipagani, taarifa zake zinapatikana katika kitabu cha
Wafalme wa pili, Nyakati wa pili na kitabu cha nabii Isaya, ambako kote anasifiwa
kama mtawala mcha Mungu, ambaye alimtegemea Mungu hata wakati wa vita mbalimbali,
Yeye alikuwa ni wa uzao wa Daudi na anayefikiriwa kama moja ya viongozi wacha
Mungu sana, hata hivyo habari yake maarufu zaidi ni pamoja na habari zake za
kuugua sana na akiwa katika kuugua huko akapokea onyo kali kupitia nabii Isaya
kuwa atengeneze mambo ya nyumba yake kwani atakufa na wala hatapona, jambo lilopelekea yeye
kumlilia Mungu na kuomba kwa machozi.
Isaya 38:1-3 “Siku hizo Hezekia aliugua,
akawa katika hatari ya kufa; na Isaya nabii, mwana wa Amozi, akaenda kwa
mfalme, akamwambia, Bwana asema hivi, Tengeneza mambo ya nyumba yako; maana
utakufa, wala hutapona. Basi Hezekia akajigeuza, akaelekeza uso wake ukutani,
akamwomba Bwana, akasema, Ee Bwana, kumbuka haya, nakusihi, kwamba nimekwenda
mbele zako katika kweli na kwa moyo mkamilifu, na kutenda yaliyo mema machoni
pako. Hezekia akalia sana sana.”
Mara kadhaa tumehubiri sana
kuhusu kisa hiki na kuonyesha nguvu za maombi na hasa maombi ya kulia sana na
machozi na tumehubiri vile vile kuhusu swala zima la Hezekia kuongezwa miaka 15,
lakini ni vigumu sana kuwasikia wahubiri wakieleza ni kwa nini mfalme huyu
mwaminifu alitakiwa atengeneze mambo ya nyumba yake? Na ni kwa nini alipewa
karipio kali kuwa hatapona bali atakufa? Tena akiwa anaumwa! Na kwanini Mungu
alikuwa ameahirisha mpango wake na kumuongezea miaka? Ni changamoto gani
ilikuweko nyuma ya karipio hili ambalo kimsingi linaweza kuwa ndio sababu ya
mkasa huu mzima! Leo Roho Mtakatifu anatuwekea wazi, kuhusiana na swala hilo.
Tutajifunza somo hili tengeneza mambo ya nyumba yako kwa kuligawa katika
vipengele vikuu vitatu muhimu vifuatavyo:-
·
Tengeneza
mambo ya nyumba yako.
·
Sababu za
kutengeneza mambo ya nyumba yako.
·
Jinsi ya
kutengeneza mambo ya nyumba yako.
Tengeneza mambo ya nyumba yako.
Isaya 38:1 “Siku hizo Hezekia aliugua,
akawa katika hatari ya kufa; na Isaya nabii, mwana wa Amozi, akaenda kwa
mfalme, akamwambia, Bwana asema hivi, Tengeneza mambo ya nyumba yako; maana
utakufa, wala hutapona.”
Hezekia aliyekuwa mfalme
mwaminifu katika utawala wa Yuda, ambaye alisababisha mabadiliko makubwa sana
ya kiimani na kuleta uamsho mkubwa sana, alitakasa Hekalu, na kuharibu
madhabahu za kipagani na ibada za sanamu, na kurejesha ibada sahihi za Mungu
aliye hai, na sikukuu za Pasaka tofauti na Ahazi baba yake, Hezekia alikuwa mtu
wa imani na maombi, mtu aliyemtegemea sana Mungu kiasi ambacho aliwahi kushinda
vita kwa kupiganiwa na Malaika baada ya kuitisha mfungo na Mungu akaingilia
kati dhidi ya majeshi ya Waashuru chini ya Senakeribu.
2Nyakati 32:20-22 “Na kwa ajili ya hayo
Hezekia mfalme, na Isaya nabii, mwana wa Amozi, wakaomba, wakalia hata
mbinguni. Naye Bwana akatuma malaika aliyewakatia mbali mashujaa wote, na
majemadari, na maakida, matuoni mwa mfalme wa Ashuru. Basi akarudia nchi yake
mwenye haya ya uso. Naye alipoingia nyumbani mwa mungu wake, wale waliotoka
viunoni mwake mwenyewe wakamwangamiza humo kwa upanga. Ndivyo Bwana
alivyomwokoa Hezekia, na wenyeji wa Yerusalemu, na mkono wa Senakeribu, mfalme
wa Ashuru, na mikononi mwa wote, akawaongoza pande zote.”
Hezekia pia alijenga mradi wa
maji maarufu kama mfereji wa Hezekia (Hezekiah’s
tunnel) unaopitisha maji chini kwa chini katika mji wa Yerusalem wa zamani
kama njia ya kujikinga na maadui endapo atazingirwa pande zote mfereji huo
maarufu wa maji uko hata siku za leo, Anatambuliwa kama moja ya wafalme maarufu
sana na mfano mzuri wa kuigwa akionyesha imani kwa Mungu na maombi na anatajwa
katika ukoo wa masihi katika agano jipya kwenye kitabu cha Mathayo kama moja ya
mababu waliomleta Yesu Kristo ulimwenguni kwa uzao wa Daudi. Ona:-
Mathayo 1:6-9 “Yese akamzaa mfalme Daudi.
Daudi akamzaa Sulemani kwa yule mke wa Uria; Sulemani akamzaa Rehoboamu;
Rehoboamu akamzaa Abiya; Abiya akamzaa Asa; Asa akamzaa Yehoshafati;
Yehoshafati akamzaa Yoramu; Yoramu akamzaa Uzia; Uzia akamzaa Yothamu; Yothamu
akamzaa Ahazi; Ahazi akamzaa Hezekia;”
Hata pamoja na sifa hizi njema
tunaona ghafla baadae alianza kuugua jipu baya sana na akiwa katika maradhi
haya mabaya na katika hali ya kuugua na kuumwa, Isaya nabii anatumwa na Mungu
kwenda kumpa ujumbe ya kwamba atakufa na wala hatapona na hivyo atengeneze
mambo ya nyumba yake, kwa nini mfalme huyu mwadilifu anatamkiwa maneno makali
hivi ya kutisha tena akiwa katika wakati wa kuumwa? Na kwa nini onyo alilopewa
na nabii linaonekana kuwa ni onyo kali sana na kisha katika namna ya kushangaza
baada ya kuomba kwake linaahirishwa kwa haraka baada ya maombi na anaongezewa
miaka 15? Nini kilipelekea Hezekia apewe onyo hili kali Tengeneza mambo ya
nyumba yako maana utakufa wala hutapona, tunajifunza nini kwenye hili?
Isaya 38:1 “Siku hizo Hezekia aliugua,
akawa katika hatari ya kufa; na Isaya nabii, mwana wa Amozi, akaenda kwa
mfalme, akamwambia, Bwana asema hivi, Tengeneza mambo ya nyumba yako; maana
utakufa, wala hutapona.”
Sababu za kutengeneza mambo ya nyumba yako.
Mungu alimtuma nabii Isaya
kumuonya Mfalme Hezekia na kumtaka atengeneze mambo ya nyumba yake, kwa ujumla
sababu za kwanini onyo hili lilikuwa kali kiasi hiki haliko wazi sana katika
Biblia Lakini unaweza kupata picha ya wazi kwamba Hezekia alikuwa na kiburi na
ubinafsi uliopitiliza ambao ungeweza kuzuia mapenzi ya Mungu, alikuwa ni mtu
aliyejihesabia haki kupita kawaida na hakuwa mtu mwenye kuamini haki ya wengine,
Mfalme Hezekia alinyooshwa katika ugonjwa mzito na angekufa kweli, lakini Mungu
hawezi kujipinga mwenyewe hivyo alimuongeza miaka 15 kwa sababu maalumu na za
msingi sana ambazo tutaziangalia hapa:-
1.
Hezekia alikuwa ni mfalme ambaye hakuwa
ameoa wala hakuwa anataka kuoa kwa mujibu wa maelezo ya tamaduni za kiyahudi
Hezekia alikuwa anaogopa kuwa akioa na kuzaa mtoto anaweza kuzaa watoto wasio
na haki na wasiomcha Mungu kama alivyo yeye na hivyo wangeweza kumuudhi Mungu,
hivyo alijiamini mwenyewe na kujihesabia haki, akidhani kuwa wengine hawataweza
kuwa kama yeye, kwa hiyo aliamini ni afadhali asioe kuliko kuoa na kuzaa watoto
watakaomkosea Mungu, Mungu alichukizwa sana na mawazo ya Hezekia kwa sababu
kama angelikufa bila kuzaa watoto, utawala wa Yuda ungekosa mfalme wa nasaba ya
Daudi jambo ambalo lingevunja ahadi ya mpango wa Mungu kwa utawala wa kudumu kwa uzao
wa Daudi;-
2Samuel 7:12-16 “Nawe
siku zako zitakapotimia, ukalala na baba zako, nitainua mzao wako nyuma yako,
atakayetoka viunoni mwako, nami nitaufanya imara ufalme wake. Yeye ndiye
atakayejenga nyumba kwa jina langu, nacho kiti cha enzi cha ufalme wake
nitakifanya imara milele. Mimi nitakuwa baba yake, naye atakuwa mwanangu;
akitenda maovu nitamwadhibu kwa fimbo ya binadamu na kwa mapigo ya wanadamu;
lakini fadhili zangu hazitamwondoka, kama vile nilivyomwondolea Sauli,
niliyemwondoa mbele yako. Na nyumba yako, na ufalme wako, vitathibitishwa
milele mbele yako. Nacho kiti chako kitafanywa imara milele.”
Mwanzo 49:8-10 “Yuda,
ndugu zako watakusifu, Mkono wako utakuwa shingoni mwa adui zako. Wana wa baba
yako watakuinamia.Yuda ni mwana-simba, Kutoka katika mawindo, mwanangu,
umepanda; Aliinama akajilaza kama simba, Na kama simba mke; ni nani
atakayemwamsha? Fimbo ya enzi haitaondoka katika Yuda, Wala mfanya sheria kati
ya miguu yake, Hata atakapokuja Yeye, mwenye milki, Ambaye mataifa watamtii.”
2.
Hezekia
alikuwa ni mfalme asiyetazama mbali; hata wakati anaumwa kwa muda mrefu
bado alikuwa hafikirii lolote kuhusu uongozi ujao, alikuwa amejaa ubinafsi
akijifikiri yeye mwenyewe, Mungu alimchungulia wakati anaumwa ikaonekana kuwa
anafikiria kumaliza vizuri na Mungu lakini hakuwaza kamwe kuandaa kiongozi
mwingine kwaajili ya kuendeleza uongozi ujao baada yake, wala hakuwaza kuwa
watu wake wataongozwaje, alikuwa mfalme mwema na wa kiroho lakini mbinafsi,
Mrithi alitakiwa kuandaliwa aone shughuli za kifalme na kujifunza maswala ya
utawala hata kabla ya kifo chake lakini yeye hakuliangalia hilo, Neno tengeneza
mambo ya nyumba yako katika lugha ya kiebrania ni “tsâvâh”
ambalo maana yake kwa kiingereza ni
appoint, au command au charge, set officially, arrange,
determine, give orders, give instruction, show direction, chagua, Amuru, weka
mtu mbadala, tangaza, andaa mrithi wako, amua, weka utaratibu, toa maelekezo,
onyesha muelekeo lilikuwa ni agizo ambalo lingemfanya Hezekia akili zake
zimrudie na afikiri kwa kina, nani anaweza kumrithi katika kiti cha ufalme
baada yake,Kama yeye atakufa nini kitafuata, Sababu zake hazikuwa za msingi kwa
Mungu, woga wake na hofu yake haikuwa na maana kwa Mungu, swala la uzao wake
watakuaje watamcha Mungu au la, halikuwa linamuhusu huwezi kuingilia na kuamua mambo ya Mungu
ndani ya mtu mwingine ni kazi ya Mungu kujua nani atakuwa mwema au itakuwaje,
ni wajibu wa Mungu kujua kuwa ajaye atafaa watu wake ama itakuwaje sio wewe,
Kwa hiyo Hezekia alitakiwa kuoa na kuzaa na kumuandaa mfalme ajaye ili baada
yake kazi ya Mungu iendelee, na uzao wa Daudi uendelee, yeye hakufanya hivyo,
Musa aliandaa mtu ambaye angeshika madaraka baada yake na Daudi aliandaa utaratibu wa mfalme ajaye na
hata majukumu yake watu walijua baada ya Daudi nini kitafuata, Mungu alimuagiza
hata Eliya kumuandaa Elisha kuwa nabii baada yake na alumuandaa hivyo mapema,
kumbe viongozi huandaliwa:-
Hesabu 27: 18-23 “Bwana
akamwambia Musa, Mtwae Yoshua, mwana wa Nuni, mtu mwenye roho ndani yake,
ukamwekee mkono wako; kisha ukamweke mbele ya Eleazari kuhani, na mbele ya
mkutano wote; ukampe mausia mbele ya macho yao. Nawe utaweka juu yake sehemu ya
heshima yako, ili mkutano wote wa wana wa Israeli wapate kutii. Naye atasimama
mbele ya Eleazari kuhani, naye atamwulizia kwa hukumu ya ile Urimu mbele za
Bwana; kwa neno lake watatoka, na kwa neno lake wataingia; yeye na wana wa
Israeli wote pamoja naye, mkutano wote pia. Musa akafanya kama Bwana
alivyomwamuru; akamtwaa Yoshua, akamweka mbele ya Eleazari kuhani, na mbele ya
mkutano wote;kisha akaweka mikono yake juu yake, akampa mausia, kama Bwana
alivyosema kwa mkono wa Musa.”
1Nyakati 28:1-9 “Kisha
Daudi akawakusanya huko Yerusalemu wakuu wote wa Israeli, wakuu wa kabila, na
maakida wa vikosi wenye kumtumikia mfalme kwa zamu, na maakida wa maelfu, na
maakida wa mamia, na wenye kutawala juu ya mali na milki za mfalme, na za
wanawe, pamoja na matowashi, na mashujaa, naam, waume mashujaa wote. Ndipo
Daudi mfalme akasimama kwa miguu yake, akasema, Nisikilizeni, ndugu zangu, na
watu wangu; Mimi nalikuwa na nia ya kuijenga nyumba ya kustarehe kwa ajili ya
sanduku la agano la Bwana, na kiti cha kuwekea miguu yake cha Mungu wetu; hata
nalikuwa nimeweka tayari kwa kujenga. Lakini Mungu akaniambia, Wewe hutajenga
nyumba kwa ajili ya jina langu, kwa sababu umekuwa mtu wa vita, nawe umemwaga
damu. Walakini Bwana, Mungu wa Israeli, alinichagua katika nyumba yote ya
babangu kuwa mfalme juu ya Israeli milele, kwa kuwa amemchagua Yuda awe mkuu;
na katika nyumba ya Yuda, alichagua nyumba ya babangu, na miongoni mwa wana wa
babangu, aliniridhia mimi ili kunitawaza niwe mfalme juu ya Israeli wote; tena
katika wana wangu wote (kwani Bwana amenipa wana wengi), amemchagua Sulemani
mwanangu ili aketi juu ya kiti cha enzi cha ufalme wa Bwana, juu ya Israeli.
Akaniambia, Sulemani, mwanao, ndiye atakayeijenga nyumba yangu na nyua zangu;
kwa kuwa nimemchagua awe mwanangu, nami nitakuwa babaye. Na ufalme wake
nitauweka imara milele, akijitia kwa bidii kuzitenda amri zangu na hukumu
zangu, kama hivi leo. Basi sasa, machoni pa Israeli wote, hilo kusanyiko la
Bwana, na masikioni pa Mungu wetu, angalieni na kuzitafuta amri zote za Bwana,
Mungu wenu, ili mpate kuimiliki nchi hii njema, na kuwarithisha wana wenu baada
yenu hata milele. Nawe, Sulemani mwanangu, mjue Mungu wa baba yako, ukamtumikie
kwa moyo mkamilifu, na kwa nia ya kumkubali; kwa kuwa Bwana hutafuta-tafuta
mioyo yote, na kuyatambua mawazo yote ya fikira; ukimtafuta, ataonekana nawe;
ukimwacha, atakutupa milele.”
1Wafalme 19:15-17 “Bwana
akamwambia, Enenda, urudi njia ya jangwa la Dameski; ukifika, mtie mafuta
Hazaeli awe mfalme wa Shamu. Na Yehu mwana wa Nimshi mtie mafuta awe mfalme wa
Israeli; na Elisha mwana wa Shafati wa Abel-Mehola mtie mafuta awe nabii mahali
pako.Na itakuwa atakayeokoka na upanga wa Hazaeli, Yehu atamwua; na
atakayeokoka na upanga wa Yehu, Elisha atamwua.”
3.
Hezekia alikuwa anaamuriwa kuweka utaratibu,
alikuwa ni kiongozi mzuri sana na mwema lakini alikuwa haandai utaratibu,
angeacha mambo hayana hata muelekeo baada ya kifo chake, je hujawahi kuona
viongozi wanaanzisha taasisi kisha wakifa wao nazo zinakufa? Watu wanaobaki
wanakuwa hawajui hata la kufanya wote wanamtegemea yeye tu, Mungu ni Mungu wa
utaratibu, Hezekia alikuwa hafiriki lolote kuhusu utaratibu utakuwaje baada
yake wakati wenzake waliomtangulia walikuwa ni watu walioweka utaratibu yeye
hata mke wa kuoa alikuwa anaogopa kuwa hatapata mke mcha Mungu na hivyo
hatakuwa na watoto wazuri wala haonyeshi mrithi wake ni nani na nini kifanyike
baada yake, kwa kufanya hivi ni kama alikuwa anazuia mpango wa Mungu wa
baadaye, kila kiongozi kuanzia ngazi ya kifamilia anapaswa kukumbuka kuwa sisi
ni wapitaji duniani, na baada ya kuongoza kwetu basi lazima aweko kiongozi
mwingine na taratibu za baadae
Yehoshafati
aliweka utaratibu mzuri sana wa kiserikali na kimaamuzi kabla ya kifo chake,
Hezekia yeye alikaa kimya tu, anaugua na haweki mipango mingine vizuri,
yalikuwa ni mawazo mabaya hakuwa kiongozi mbaya alimcha Mungu lakini hakuwa
akifikiri zaidi ya mambo katika jicho la kiungu, hakuwaza kazi ya Mungu baada
yake itakuwaje, kiongozi ambaye angemrithi angekosa hata pa kuanzia hajui
aanzie wapi, hii ilikuwa changamoto yake ona mfano wa Yehoshafati yeye aliweka
taratibu nzuri za kimaongozi na kiserikali ona!
2Nyakati 19:4-11 “Na
Yehoshafati akakaa Yerusalemu; akatoka tena kwenda kati ya watu toka Beer-sheba
mpaka milima ya Efraimu, akawarudisha kwa Bwana, Mungu wa baba zao.
Akasimamisha makadhi katika nchi, katikati ya miji yote yenye maboma ya Yuda,
mji kwa mji; akawaambia hao makadhi, Angalieni myafanyayo; kwa kuwa hammfanyii
mwanadamu hukumu, ila Bwana; naye yupo pamoja nanyi katika neno la hukumu. Basi
sasa hofu ya Bwana na iwe juu yenu; angalieni mkaifanye; kwa maana kwa Bwana,
Mungu wetu, hapana uovu, wala kujali nafsi za watu, wala kupokea zawadi.Tena
katika Yerusalemu Yehoshafati akasimamisha wa Walawi na makuhani, na wakuu wa
mbari za mababa wa Israeli wawe kwa hukumu ya Bwana, na kwa mateto. Nao
wakarudi Yerusalemu. Akawaagiza, akasema, Ndivyo mtakavyotenda kwa hofu ya
Bwana, kwa uaminifu, na kwa moyo kamili. Na kila mara watakapowajia na teto
ndugu zenu wakaao mijini mwao, kati ya damu na damu, kati ya torati na amri,
sheria na hukumu, mtawaonya, wasiingie hatiani mbele za Bwana, mkajiliwa na
ghadhabu ninyi na ndugu zenu; fanyeni haya wala hamtakuwa na hatia.Tena
angalieni, Amaria, kuhani mkuu, yu juu yenu kwa maneno yote ya Bwana; naye
Zebadia, mwana wa Ishmaeli, jemadari wa nyumba ya Yuda, kwa maneno yote ya
mfalme; Walawi nao watakuwa wasimamizi mbele yenu. Jitieni nguvu, mtende, naye
Bwana awe pamoja nao walio wema.”
Hata hivyo jambo jema ni kuwa
baada ya maonyo Hezekia aliutafuta uso wa Mungu, aligeukia ukutani na kutafuta
uso wa Mungu, aliomba na kulia sana alijutia tabia yake na ubinafsi wake
aliokuwa nao, alimkumbusha Mungu jinsi alivyotembea kwa uaminifu alilia na
kujutia kosa lake na Mungu alimrehemu haraka na kumuongezea Muda wa kufanya
maandalizi, ni katika muda huu wa nyongeza ndipo alipooa na ndani ya miaka
mitatu alizaliwa Manase
Isaya 38:2-6 “Basi Hezekia akajigeuza,
akaelekeza uso wake ukutani, akamwomba Bwana, akasema, Ee Bwana, kumbuka haya,
nakusihi, kwamba nimekwenda mbele zako katika kweli na kwa moyo mkamilifu, na
kutenda yaliyo mema machoni pako. Hezekia akalia sana sana. Ikawa, neno la
Bwana likamjia Isaya, kusema, Enenda ukamwambie Hezekia, Bwana, Mungu wa Daudi,
baba yako, asema hivi, Mimi nimeyasikia maombi yako, nimeyaona machozi yako;
tazama, nitaziongeza siku zako, kiasi cha miaka kumi na mitano. Nami nitakuokoa
wewe, na mji huu, na mkono wa mfalme wa Ashuru, nami nitaulinda mji huu.”
Jinsi ya kutengeneza mambo ya nyumba yako
Kuna mambo kadhaa ya kujifunza
kutoka kwa maisha ya Hezekia na mkasa huu, waalimu wa Kiyahudi wanaelezea ya
kuwa Hezekia alioa haraka sana baada ya kuponywa na alimuoa mwanamke ambaye
alikuwa ni binti wa nabii Isaya baada ya kukemewa na kuponywa, Nabii Isaya
alimuelekeza jinsi ya kutengeneza mambo ya nyumba yake alitakiwa kuoa haraka
hata bila kujali kuwa wazao wake watakuwa wema au wabaya, hakutakiwa kuogopa
mambo yajayo wala kuharibu yanayobaki,alitakiwa kuweka utaratibu na kuandaa
mrithi wa kifalme kwaajili ya Daudi mtumishi wa Mungu ili ahadi ya Mungu
itimie, Mfalme Hezekia alimuoa “Hefsiba”
ambaye alikuwa ni binti wa nabii Isaya
na miaka mitatu baada ya kuponywa kwake walifanikiwa kumpata mtoto
aliyeitwa Manase, huyu akawa mfalme mpya hata hivyo akawa muovu sana kuliko
wafalme wote katika Yuda, aliwahi kumtoa mwane sadaka ya kuteketezwa,akajihusha
na waganga na wachawi na ibada za sanamu na kuabudu malaika na machukizo ya
kila aina
Isaya 62:4-5 “Hutaitwa tena Aliyeachwa,
wala nchi yako haitaitwa tena, Ukiwa; bali utaitwa Hefsiba; na nchi yako Beula;
kwa kuwa Bwana anakufurahia, na nchi yako itaolewa.Maana kama vile kijana
amwoavyo mwanamwali, ndivyo wana wako watakavyokuoa wewe; na kama vile bwana
arusi amfurahiavyo bibi arusi, ndivyo Mungu wako atakavyokufurahia wewe.”
2Wafalme 21:1-6 “Manase alikuwa na umri wa
miaka kumi na miwili alipoanza kutawala; akatawala miaka hamsini na mitano
katika Yerusalemu, na jina la mamaye aliitwa Hefziba. Akafanya yaliyo mabaya
machoni pa Bwana, sawasawa na machukizo ya mataifa, aliowafukuza Bwana mbele ya
wana wa Israeli. Kwa maana akapajenga tena mahali pa juu alipopaharibu Hezekia
baba yake; akamjengea Baali madhabahu, akafanya Ashera kama alivyofanya Ahabu
mfalme wa Israeli. Akajiinama mbele ya jeshi lote la mbinguni na kulitumikia.
Akazijenga madhabahu ndani ya nyumba ya Bwana, napo ndipo alipopanena Bwana,
Katika Yerusalemu nitaliweka jina langu. Akajenga madhabahu kwa ajili ya jeshi
lote la mbinguni katika behewa mbili za nyumba ya Bwana. Akampitisha mwanawe
motoni, akatazama bao, akafanya uganga, akajishughulisha na hao wenye pepo wa
utambuzi, na wachawi; akafanya mabaya mengi machoni pa Bwana, hata kumkasirisha.”
Mambo ya kujifunza:-
1.
Hakuna mtu mwenye uhakika na kesho, kesho
iko mikononi mwa Mungu tu, Hezekia ingawa alikuwa mwema lakini bado alikumbushwa
kuwa kuna kifo na akapokea taarifa hizo bila kutarajia, kwa kawaida huwa
tunajisahau kama wanadamu tunadhani tutaendelea kuwepo siku zote, uzima huu
unatupa kiburi, pumzi hii inatufanya tufikiri ubovu ni wa wengine na kifo ni
cha wengine, tunajifikiri sisi tu, hatufurahii kuandaa wengine, hatufikirii
uhai wa taasisi wakati ujao, maisha ya mwanadamu ni kama mvuke tu, na kama ua
la kondeni, usisahau kuwa kuna kifo, hata Musa alikumbushwa na Mungu akamuandaa
Yoshua, Eliya alimuandaa Elisha, Paulo Mtume alimuanda Timotheo na wengine, wewe
na mimi tunataka tukizimika wengine waone giza tu hicho ni kiburi na sio mpango
wa Mungu.
Ayubu 14:1-2 “Mwanadamu
aliyezaliwa na mwanamke Siku zake za kuishi si nyingi, naye hujaa taabu. Yeye
huchanua kama vile ua, kisha hukatwa; Hukimbia kama kivuli, wala hakai kamwe”
2.
Kutengeneza mambo ya nyumba yako sio agizo
kwa Hezekia tu, ni agizo la kila mtu, iandae familia yako, andaa waandae
kwaajili ya mambo yajayo, andaa mahusiano mazuri na watu, andaa kwa kuondoa madeni ya kimwili na kiroho
hakikisha yanalipwa, kumbuka kuweka maagizo, kumbuka kuna maisha baada ya kazi,
kuna maisha baada ya kustaafu, kuna kutafuta kwa bidii kuwa na amani na watu
wote, wewe na mimi hatutakuwepo milele tuache ubinafsi, Ondoa kinyongo chako
moyoni, usijiweke katika nafasi ya Mungu, acha kuhukumu wengine na kudhani kuwa
uko wewe peke yako Mungu anao watu wengi sana na anaweza kuwatumia, lakini ni
wajibu wetu kuwaandaa na wengine waweze kutimiza hivyo Majukumu ya mbeleni.
Kutokujiayarisha
kwa maswala ya Mungu kunaitwa upumbavu katika maandiko, lakini tukihesabu siku
zetu fupi za kuweko duniani na tukazitumie vizuri ikiwa ni pamoja na kuwa
tayari tunaitwa wenye hekima na akili
Zaburi 90:10-12 “Siku
za miaka yetu ni miaka sabini, Na ikiwa tuna nguvu miaka themanini; Na kiburi
chake ni taabu na ubatili, Maana chapita upesi tukatokomea mara.Ni nani aujuaye
uweza wa hasira yako? Na ghadhabu yako kama ipasavyo kicho chako? Basi,
utujulishe kuzihesabu siku zetu, Tujipatie moyo wa hekima.”
Luka 12:15-21 “Akawaambia,
Angalieni, jilindeni na choyo, maana uzima wa mtu haumo katika wingi wa vitu
vyake alivyo navyo. Akawaambia mithali, akisema, Shamba la mtu mmoja tajiri
lilikuwa limezaa sana; akaanza kuwaza moyoni mwake, akisema, Nifanyeje? Maana
sina pa kuyaweka akiba mavuno yangu. Akasema, Nitafanya hivi; nitazivunja ghala
zangu, nijenge nyingine kubwa zaidi, na humo nitaweka nafaka yangu yote na vitu
vyangu. Kisha, nitajiambia, Ee nafsi yangu, una vitu vyema vingi ulivyojiwekea
akiba kwa miaka mingi; pumzika basi, ule, unywe, ufurahi. Lakini Mungu
akamwambia, Mpumbavu wewe, usiku huu wa leo wanataka roho yako! Na vitu
ulivyojiwekea tayari vitakuwa vya nani? Ndivyo alivyo mtu ajiwekeaye nafsi yake
akiba, asijitajirishe kwa Mungu.”
3.
Fanya mambo yao yote kwa uaminifu, Hezekia alikuwa
mwaminifu na uaminifu wake ulikuja kumkomboa baadaye, Mungu alimuongezea umri
kwa sababu alikuwa mwaminifu na alikubali mapenzi ya Mungu baada ya kuponywa
jipu lake sugu, kumbuka wakati wowote unaweza kufa, hata kama wewe u mwema usisubiri
tangazo la kifo ndipo uanze kujiandaa, je umeandaa watoto wako wa kiroho,
umeandaa viongozi wajao, ndoa yako iko vizuri, watoto wako wamefundishwa njia
za Bwana, je umesamehe waliokukosea, je una Amani na watu wote, je kwa Mungu
uhusiano wako uko salama, Geuka ukutani leo ujifanyie tathimini wewe na Mungu
wako kama mambo yako yako sawa sawa au la kama kuna kwa kutengeneza tubu,
tengeneza mambo ya nyumba yako
2Petro 3:9 “Bwana
hakawii kuitimiza ahadi yake, kama wengine wanavyokudhani kukawia, bali
huvumilia kwenu, maana hapendi mtu ye yote apotee, bali wote wafikilie toba.”
4.
Unyenyekevu ni nyenzo ya thamani kubwa, - Kuugua
kwa Hezekia kulimkumbusha swala zima la unyenyekevu, alipopewa taarifa za
kutokupona alionyesha ya kuwa anamtegemea Mungu, alijinyenyekeza kwa Mungu
wake, ni mfalme lakini aliamini katika maombi, alitubu na hakujihesabia haki,
alipopona na kuongezwa maiaka 15 aliitumia vema kukamilisha kazi iliyosalia
mbele yake kwa uaminifu, Hezekia alijifunza wazi kuwa iko sauti ya Mungu wakati
tunapougua, lazima tujifunze na kujua kuwa Mungu anataka jambo gani lifanyike
wakati wa kuugua kwetu na Hezekia aliyajua mapenzi ya Mungu na alijua dhambi
zake akatubu
Isaya 38:17-20 “Tazama;
nalikuwa na uchungu mwingi kwa ajili ya amani yangu; Lakini kwa kunipenda
umeniokoa na shimo la uharibifu; Kwa maana umezitupa dhambi zangu zote nyuma
yako. Kwa kuwa kuzimu hakuwezi kukusifu; mauti haiwezi kukuadhimisha; Wale
washukao shimoni hawawezi kuitarajia kweli yako. Aliye hai, naam, aliye hai,
ndiye atakayekusifu, kama mimi leo; Baba atawajulisha watoto kweli yako.Bwana
yu tayari kunipa wokovu. Basi, kwa vinubi tutaziimba nyimbo zangu, Siku zote za
maisha yetu nyumbani mwa Bwana.”
Na. Rev, Innocent Samuel Kamote
Mkuu wa wajenzi mwenye Hekima

Hakuna maoni:
Chapisha Maoni