Jumapili, 14 Desemba 2025

Siku za miaka ya kusafiri kwangu!


Mwanzo 47:7-9 “Yusufu akamleta Yakobo babaye ndani akamweka mbele ya Farao. Yakobo akambariki Farao. Farao akamwuliza Yakobo, Je! Siku za miaka ya maisha yako ni ngapi? Yakobo akamjibu Farao, Siku za miaka ya kusafiri kwangu ni mia na thelathini; siku za miaka ya maisha yangu zimekuwa chache, tena za taabu, wala hazikufikilia siku za miaka ya maisha ya baba zangu katika siku za kusafiri kwao.”




Utangulizi:

Ni muhimu kufahamu kuwa maisha yetu hapa duniani yanafananishwa na safari, siku zetu za kuishi ni chache na tena zimejaa taabu sana, Maisha yetu yamejaa mabadiliko mengi sana na changamoto nyingi sana za kimwili na kiroho, kwa ujumla maisha yetu duniani ni ya kitambo kifupi sana ingawaje yana kusudi kubwa la Mungu na maana kubwa sana ya kiroho, Na ndio maana Yakobo alielewa wazi kuwa maisha yake duniani ni kama safari, anapita katika hii dunia kama mgeni na mpitaji tu, Yakobo alikuwa na ufahamu kuwa dunia hii sio nyumbani kwetu na kwamba hata kama ataishi maisha merefu kiasi gani bado miaka hiyo itakuwa ni miaka ya kusafiri kwake tu. Hivi ndivyo maandiko yanavyotukumbusha hata leo ili tuishi vizuri tukiwa na uhusiano mzuri na Amani kwa Mungu na wanadamu wote!

1 Petro 2:11-12 “Wapenzi, nawasihi kama wapitaji na wasafiri, ziepukeni tamaa za mwili zipiganazo na roho. Mwe na mwenendo mzuri kati ya Mataifa, ili, iwapo huwasingizia kuwa watenda mabaya, wayatazamapo matendo yenu mazuri, wamtukuze Mungu siku ya kujiliwa.”

Miaka ya kusafiri ni usemi (Metaphor) unaokazia kuwa maisha ni safari ya mchakato wenye kutupa uzoefu, mafunzo, kukua, kuelewa, kukomaa, kuongeza ufahamu na maarifa na kukutana na mambo chanya na mambo hasi, kutuchonga, kuuelewa ulimwengu na zaidi sana kuelewa kusudi la kuwepo kwetu, kwa utukufu wa Mungu Baba, hata hivyo maisha ni ya kitambo/yaani ni ya muda mfupi, sana na kwa sababu hiyo tunatiwa moyo kukabiliana na changamoto zote na kuzihesabu kuwa ni nafasi ya kipekee ya kutuandaa kwaajili ya maisha yajayo, Maisha ni safari kwa sababu hapa duniani sio mwisho na hatujafika na badala yake tunapita tu. Leo tutachukua muda basi kutafakari somo hili muhimu kwetu “Siku za miaka ya kusafiri kwangu” kwa kuzingatia vipengele vitatu vifuatavyo:-

·         Siku za miaka ya kusafiri kwangu.

·         Siku za miaka ya maisha yangu zimekuwa chache, tena za taabu.

·         Wakristo kama wasafiri  
              

Siku za miaka ya kusafiri kwangu

Mwanzo 47:7-9 “Yusufu akamleta Yakobo babaye ndani akamweka mbele ya Farao. Yakobo akambariki Farao. Farao akamwuliza Yakobo, Je! Siku za miaka ya maisha yako ni ngapi? Yakobo akamjibu Farao, Siku za miaka ya kusafiri kwangu ni mia na thelathini; siku za miaka ya maisha yangu zimekuwa chache, tena za taabu, wala hazikufikilia siku za miaka ya maisha ya baba zangu katika siku za kusafiri kwao.”

Ni muhimu kujifunza na kutafakari jinsi ambavyo Yakobo anayachukulia maisha kama safari, Maisha ni safari kweli ya kimwili na kiroho, Safari hii inakabiliwa na maswala mengi chanya na hasi lakini zaidi sana nyakati muhimu za kufanya maamuzi ambayo yataamua hatima yetu ya baadaye, ndani ya maisha tutapimwa imani, utii, na changamoto za kimaisha zitakazolazimisha maisha yetu yawe na mabadiliko kadhaa na kuzaa uvumilivu utakaotusaidia kuwa na uwepo wa Mungu na ukomavu.

Yakobo anaonyesha kuwa sio yeye tu alikuwa katika safari ya maisha lakini hata baba zake yaani Ibrahimu na Isaka nao walikuwa katika kusafiri kwao, hivyo Ibrahimu, na Isaka na Yakobo waliishi duniani kama wasafiri na wapitaji duniani, hawakuwa na makazi ya kudumu, waliishi kwa Imani, walijitambua kuwa hapa duniani wao ni wapitaji tu.

Waebrania 11:13-16 “Hawa wote wakafa katika imani, wasijazipokea zile ahadi, bali wakaziona tokea mbali na kuzishangilia, na kukiri kwamba walikuwa wageni, na wasafiri juu ya nchi. Maana hao wasemao maneno kama hayo waonyesha wazi kwamba wanatafuta nchi yao wenyewe. Na kama wangaliikumbuka nchi ile waliyotoka, wangalipata nafasi ya kurejea. Lakini sasa waitamani nchi iliyo bora, yaani, ya mbinguni. Kwa hiyo Mungu haoni haya kuitwa Mungu wao; maana amewatengenezea mji.”

Yakobo anahesabu miaka ya kukaa duniani kama miaka ya safari tu, Yeye na wazazi wake waliishi hivyo, hii ni kwa sababu hawakuishi katika nyumba za kudumu kama tunavyoishi leo, maisha yao yalikuwa ya kutanga tanga na kuhama hama (Nomads), kwa hiyo hawakuwa na makazi ya kudumu, waliishi duniani kama wapitaji wakiashiria ukweli halisi wa maisha ya kuwa maisha ni safari, na imejaa mabadiliko ya iana mbalimbali kimwili na kiroho, wakipitia changamoto nyingi na majaribu mengi, pamoja na baraka za Mungu, lakini maisha ya kawaida ya kibinadamu yana changamoto nyingi wao walikuwa ni mfano tu wa kutukumbusha sisi tunaoishi leo kwamba tuko safarini, na kuwa duniani tunapita tu, tuko hapa katika hali ya ugeni tu na dunia sio nyumbani kwetu kwa kudumu, maisha ya mwanadamu ni ya muda tu, ujumbe wake Yakobo na majibu yake kwa Farao yalikuwa  ni  mauhubiri tosha kumjulisha Farao kuwa wanadamu wote hapa dunia ni wanasafiri akiwepo yeye aliyekuwa na madaraka makubwa duniani kwa wakati ule, Yakobo alitaka hili lifike akilini kwa mtu huyu mkubwa kumkumbusha kuwa Pamoja na mamlaka yake kubwa na nguvu alizo nazo anapaswa kukumbuka kuwa siku za miaka yetu ni siku za miaka ya kusafiri kwetu tu na hakuna cha kudumu duniani!

Waebrania 11:8-9.“Kwa imani Ibrahimu alipoitwa aliitika, atoke aende mahali pale atakapopapata kuwa urithi; akatoka asijue aendako. Kwa imani alikaa ugenini katika ile nchi ya ahadi, kama katika nchi isiyo yake, akikaa katika hema pamoja na Isaka na Yakobo, warithi pamoja naye wa ahadi ile ile.”

Kila mwanadamu mwenye akili timamu anapaswa kukumbuka kuwa maisha haya ni “temporally” ni ya muda tu tunapita kwa kasi sana na kwa sababu hiyo hatuna budi kuishi kwa Amani na wenzetu na kuwafanyia watu mambo mema, tusiwafanyie watu ubaya, wala tusiwawekee watu kinyongo, na kujilimbikizia mali na madaraka kana kwamba sisi ni watawala wa kifalme, watu wengi hujisahau katika hili, Yakobo alikuwa amebarikiwa sana lakini hakusahau kuwa yeye ni msafiri, tuishi na watu vizuri, isifikie wakati watu wakafurahia kufa kwetu au kuugua kwetu, badala yake watuombolezee, siku hizi linaanza kuwa jambo la kawaida watu kufurahia kifo cha watu wengine kana kwamba wao hawatakufa, lakini sababu kubwa ni kuwa watu hao waliishi bila ya kujali wengine, au waliumiza wengine kwaajili ya ubinafsi na mafanikio yao, na wengine, walijisahau kuwa wao wanapita tu, kila kitu duniani ni cha muda tu na maisha kwa ujumla yana masomo mengi ya kutufunza! Na la muhimu sisi ni wasafiri na tuko duniani kwa muda!, acha kinyongo, acha kuhukumu wengine, acha ubinafsi, acha kinyongo, tafuta kwa bidi Amani na wote

Siku za miaka ya maisha yangu zimekuwa chache, tena za taabu.

Yakobo wakati anashuka Misri na kuonana na Farao wakati huu alikuwa na miaka 130 na mpaka anafariki alikuwa na umri wa miaka 147 tu, kwa msingi huo aliishi Misri kwa muda wa miaka kama  17 hivi, Yakobo anaziona siku hizi kuwa ni chache sana, Ibrahimu aliishi miaka 175, wakati Isaka aliishi miaka 180. Kwa hiyo Yakobo anayaona maisha yake kuwa mafupi na yaliyojaa taabu sana kuliko maisha ya baba zake, na pia ingawa hakuwa anajua ataishi umri gani lakini alijitabiria kuwa siku zake ni chache na zilizojaa taabu sana kuliko siku za baba zake, yaani Isaka na Ibrahimu, Yakobo alipanda milima na mabonde akipambana na maisha yaliyojaa ugumu wa maswala mbalimbali kama:

1.       Migogoro ya kifamilia – Yakobo alilazimika kukimbia nyumbani siku za maisha ya ujana wake na kuishi mbali na baba na mama kwaajili ya kumkimbia kaka yake, Esau, hayakuwa maisha ya kawaida, tabia yake ya hila na kuutumia upole wa kaka yake kwa faida zake mwenyewe uliweza kuongeza ugumu wa maisha na kumfanya kuwa mbali na wapendwa wake wa karibu uko uwezekano kuwa Yakobo Hakuonana na Rebeka tena mpaka kifo kwajili ya tukio hili.

 

Mwanzo 27:41-45 “Esau akamchukia Yakobo kwa ajili ya ule mbaraka babaye aliombarikia. Esau akasema moyoni mwake, Siku za kumlilia baba yangu zinakaribia, ndipo nitakapomwua ndugu yangu Yakobo. Rebeka akaarifiwa maneno ya Esau, mwanawe mkubwa. Akapeleka mtu kumwita Yakobo, mwanawe mdogo, akamwambia, Tazama, katika habari zako Esau, ndugu yako, anajifariji moyo wake, maana anakusudia kukuua. Na sasa, mwanangu, sikia sauti yangu, uondoke, ukimbilie kwa Labani, ndugu yangu huko Harani; ukae kwake siku chache, hata ghadhabu ya ndugu yako igeuke; hata ikuondokee ghadhabu ya ndugu yako, akasahau uliyomtenda. Ndipo nitakapopeleka watu kukuchukua kutoka huko. Kwa nini nifiwe nanyi nyote wawili siku moja?”             

 

2.       Dhuluma na ukatili kutoka kwa mjomba – Yakobo alipokuwa akifanya kazi kwa mjomba wake, ni ukweli usiopingika kuwa Yakobo alikuwa na mjomba aliyejaa hila zaidi kuliko yeye, aliishi na mjomba katili, alimdanganya katika maswala ya ndoa na kuishia kumtumikisha, lakini alibadili-badili maswala ya mkataba wa mshahara wake zaidi ya mara kumi, siku chache zilizokadiriwa na kudhaniwa na Rebeka, zikawa ni miaka mingi ya kitumwa uko uwezekano kuwa alikaa ugenini kwa mjomba wake kwa miaka 20 akidhulumiwa tu

 

Mwanzo 29:18-27 “Yakobo akampenda Raheli akasema, Nitakutumikia miaka saba kwa kumpata Raheli, binti yako mdogo. Labani akasema, Afadhali nikupe wewe kuliko mtu mwingine; kaa kwangu. Yakobo akatumika miaka saba kwa kumpata Raheli. Ikawa machoni pake kama siku chache tu kwa vile alivyompenda. Yakobo akamwambia Labani, Nipe mke wangu, maana siku zangu zimetimia; niingie kwake. Labani akakusanya watu wote wa mahali pale, akafanya karamu. Ikawa wakati wa jioni akamtwaa Lea, binti yake, akamletea Yakobo, naye akaingia kwake. Labani akampa Lea mjakazi wake Zilpa, awe mjakazi wake. Ikawa, kulipokuwa asubuhi, kumbe! Ni Lea. Akamwambia Labani, Nini hii uliyonitenda? Sikukutumikia kwa Raheli? Mbona umenidanganya? Labani akasema, Havitendeki hivi kwetu, kumtoa mdogo kabla ya mkubwa; timiza siku zake saba, nasi tutakupa huyu naye kwa utumishi utakaonitumikia, miaka saba mingine.”

 

Mwanzo 31:1-9 “Basi Yakobo akasikia maneno ya wana wa Labani, wakisema, Yakobo amechukua mali yote ya baba yetu; na kwa mali ya baba yetu amepata fahari hii yote. Yakobo akaona uso wa Labani, ya kuwa hakumtazama vema kama jana na juzi.  BWANA akamwambia Yakobo, Urudi mpaka nchi ya baba zako na kwa jamaa zako, nami nitakuwa pamoja nawe. Yakobo akatuma watu, akawaita Raheli na Lea waje nyikani kwenye wanyama wake. Akawaambia, Naona uso wa baba yenu, kwamba hanitazami vema kama jana na juzi. Lakini Mungu wa baba yangu amekuwa pamoja nami. Nanyi mmejua ya kwamba kwa nguvu zangu zote nimemtumikia baba yenu. Na baba yenu amenidanganya, akabadili mshahara wangu mara kumi; lakini Mungu hakumwacha kunidhuru. Aliposema, Walio na madoadoa watakuwa mshahara wako, wanyama wote wakazaa madoadoa. Aliposema, Walio na milia watakuwa mshahara wako, ndipo wanyama wote wakazaa wenye milia. Hivi Mungu akamnyang'anya mali yake baba yenu, na kunipa mimi.”

 

3.       Mateso katika familia yake – Yakobo alikutana na changamoto kutoka katika familia yake mwenyewe, watoto wake waliokuwa wakichukiana wao kwa wao, walimuuza ndugu yao Yusufu kijana wake mpendwa na kumdanganya kuwa amefariki, Yakobo aliomboleza sana akijua kuwa mwanae atakuwa amefariki, hii ilizidisha shida na huzuni kubwa katika maisha yake, nadhani walifanya msiba na kuzika nguo lakini kumbe alikuwa amedanganywa tena!

 

Mwanzo 37:31-35 “Wakaitwaa kanzu ya Yusufu, wakachinja mwana-mbuzi, na kuichovya kanzu katika damu. Wakaenda nayo ile kanzu ndefu, wakamletea baba yao, wakasema, Tumeona hii; basi, utambue kama kanzu hii ni ya mwanao, ama siyo. Akaitambua, akasema, Ndiyo kanzu ya mwanangu, mnyama mkali amemla; bila shaka Yusufu ameraruliwa. Yakobo akararua mavazi yake, akajivika gunia viunoni, na kumlilia mwanawe siku nyingi. Wanawe wote, na binti zake wote, wakaondoka wamtulize, lakini akakataa kutulizwa, akasema, La! Nitamshukia mwanangu, nikisikitika, hata kuzimu. Baba yake akamlilia.”

 

4.       Njaa iliyosababisha safari Misri – Pamoja na mapito kadhaa wa kadhaa ilimlazimu kusafiri na kuiacha nchi ya ahadi akiwa na umri mkubwa 130, anakumbwa na njaa inayowalazimisha kushuka Misri kwaajili ya chakula na wito wa mwanaye Yusufu, Ingawa Abrahamu na Isaka walikutana na changamoto mbalimbali katika maisha, Yakobo anahisi maisha yake yalikuwa magumu zaidi kuliko wao  kwa sababu ya wingi wa mateso na maumivu na migogoro ya kifamilia aliyoipitia, Hata hivyo katika hali isiyokuwa ya kawaida Mungu alimtia moyo kushuka Misri na aliambiwa na Mungu kuwa atakuwa pamoja naye, atafia huko mikononi mwa Yusufu

 

Mwanzo 46:2-4 “Mungu akanena na Israeli katika ndoto ya usiku, akasema, Yakobo, Yakobo. Akasema, Mimi hapa. Akasema, Mimi ni Mungu, Mungu wa baba yako, usiogope kushuka mpaka Misri; maana nitakufanya uwe taifa kubwa huko. Mimi nitashuka pamoja nawe mpaka Misri; nami nitakupandisha tena bila shaka; na Yusufu ataweka mkono wake juu ya macho yako.”

Wakristo kama wasafiri               

Kimsingi yako maswala mengi ya kujifunza kutoka kwa Yakobo na mtazamo wake wa maisha kama safari

1.       Tunajifunza kuwa maisha yetu ni ya muda – Haijalishi utaishi duniani kwa muda gani lakini vyovyote iwavyo maisha ni ya muda mfupi sana na maandiko yako wazi kuhusiana na jambo hili, na kuonyesha ufupi wa maisha ikionyesha mifano ya maua, mvuke, majani, usingizi na kadhalika

 

Zaburi 90:5-6 “Wawagharikisha, huwa kama usingizi, Asubuhi huwa kama majani yameayo. Asubuhi yachipuka na kumea, Jioni yakatika na kukauka.”

 

Yakobo 4:13-15 “Haya basi, ninyi msemao, Leo au kesho tutaingia katika mji fulani na kukaa humo mwaka mzima, na kufanya biashara na kupata faida; walakini hamjui yatakayokuwako kesho. Uzima wenu ni nini? Maana ninyi ni mvuke uonekanao kwa kitambo, kisha hutoweka. Badala ya kusema, Bwana akipenda, tutakuwa hai na kufanya hivi au hivi.”

 

2.       Tunajifunza kumtegemea Mungu na neno lake – Wakati wote wa mahangaiko yake Yakobo pamoja na safari zake alizokuwa akizunguka duniani Mungu alimtokea mara kwa mara na kumuonyesha dhahiri kuwa atakuwa pamoja naye, wakati mwingine katika maisha yako utahangaika huku na huko na unaweza ukafikiri kuwa labda Mungu hako pamoja nawe lakini nataka nikudhihirishie kuwa yuko pamoja nawe, haijalishi ulikoenda ni utumwani au unakutana na shida gani kama Mungu alivyomuongoza Yakobo atakuongoza na wewe pia katika safari yako ya maisha, changamoto za maisha na ugumu wake ni jambo la kawaida.

 

Mwanzo 28:10-15 “Yakobo akatoka Beer-sheba, kwenda Harani. Akafika mahali fulani akakaa huko usiku kucha, maana jua lilikuwa limekuchwa; akatwaa jiwe moja la mahali pale akaliweka chini ya kichwa chake, akalala usingizi pale pale. Akaota ndoto; na tazama, ngazi imesimamishwa juu ya nchi, na ncha yake yafika mbinguni. Tena, tazama, malaika wa Mungu wanapanda, na kushuka juu yake. Na tazama, BWANA amesimama juu yake, akasema, Mimi ni BWANA, Mungu wa Ibrahimu baba yako, na Mungu wa Isaka; nchi hii uilalayo nitakupa wewe na uzao wako. Na uzao wako utakuwa kama mavumbi ya nchi, nawe utaenea upande wa magharibi, na mashariki, na kaskazini, na kusini; na katika wewe, na katika uzao wako, jamaa zote za dunia watabarikiwa. Na tazama, mimi nipo pamoja nawe, nitakulinda kila uendako, nami nitakuleta tena mpaka nchi hii, kwa maana sitakuacha, hata nitakapokufanyia hayo niliyokuambia.”              

Mwanzo 46:2-4 “Mungu akanena na Israeli katika ndoto ya usiku, akasema, Yakobo, Yakobo. Akasema, Mimi hapa. Akasema, Mimi ni Mungu, Mungu wa baba yako, usiogope kushuka mpaka Misri; maana nitakufanya uwe taifa kubwa huko. Mimi nitashuka pamoja nawe mpaka Misri; nami nitakupandisha tena bila shaka; na Yusufu ataweka mkono wake juu ya macho yako.”

 

Zaburi 119:105 “Neno lako ni taa ya miguu yangu, Na mwanga wa njia yangu.”

 

3.       Tunajifunza kujitayarisha kwa Mungu – Kwa kuwa maisha ni ya muda tu maana yake pamoja na kupanga na kuweka maono na mikakati ya kibinadamu, kamwe tusiache kujitayarisha kwa Mungu, maandiko yanamuita mtun anayejiwekea mikakati ya kidunia na kuacha kujitayarisha kwa Mungu kama mtu mpumbavu, kwa sababu hiyo Mungu atupe moyo wa hekima ili tujue itupasavyo kuhesabu siku zetu.

 

Luka 12:16-21 “Akawaambia mithali, akisema, Shamba la mtu mmoja tajiri lilikuwa limezaa sana; akaanza kuwaza moyoni mwake, akisema, Nifanyeje? Maana sina pa kuyaweka akiba mavuno yangu. Akasema, Nitafanya hivi; nitazivunja ghala zangu, nijenge nyingine kubwa zaidi, na humo nitaweka nafaka yangu yote na vitu vyangu. Kisha, nitajiambia, Ee nafsi yangu, una vitu vyema vingi ulivyojiwekea akiba kwa miaka mingi; pumzika basi, ule, unywe, ufurahi. Lakini Mungu akamwambia, Mpumbavu wewe, usiku huu wa leo wanataka roho yako! Na vitu ulivyojiwekea tayari vitakuwa vya nani? Ndivyo alivyo mtu ajiwekeaye nafsi yake akiba, asijitajirishe kwa Mungu.”

 

4.       Tunajifunza kuwa tayari kukabiliana na magumu – Kuwa mtu wa Mungu kamwe hakukufanyi wewe usikutane na magumu hapa duniani, Yakobo alikuwa mtu wa Mungu na Mungu alimbariki sana lakini hata hivyo maisha yake au miaka ya kusafiri kwake duniani ilijaa taabu kuliko ya siku za baba zake kama anavyosema, hii inatufundisha na kutuimarisha kuwa, kuwa mtu wa Mungu hakutazuia wewe kukutana na magumu, lakini pamoja na hayo tusiache kumcha Mungu na kuwa na uhusiano naye, Yakobo alikutana na changamoto nyingi lakini aliendelea kuwa na uhusiano na Mungu na kuwa mvumilivu na mwenye subira na Mungu akawa pamoja naye.  

 

Waebrania 13:5-6 “Msiwe na tabia ya kupenda fedha; mwe radhi na vitu mlivyo navyo; kwa kuwa yeye mwenyewe amesema, Sitakupungukia kabisa, wala sitakuacha kabisa. Hata twathubutu kusema, Bwana ndiye anisaidiaye, sitaogopa; Mwanadamu atanitenda nini?

 

5.       Tunajifunza kuishi kwa viwango – Wasafiri na wapitaji hawaishi kwa viwango vya ugenini na badala yake huishi kwa viwango vya nchi zao, sisi wenyeji wetu uko mbinguni na kwasababu hiyo kamwe hatupaswi kuishi sawa na watu wa dunia hii, wala kufungwa na mambo ya dunia hii, badala yake tuishi sawa na viwango vya kule tunakokwenda.

 

Warumi 12:1-2 “Basi, ndugu zangu, nawasihi, kwa huruma zake Mungu, itoeni miili yenu iwe dhabihu iliyo hai, takatifu, ya kumpendeza Mungu, ndiyo ibada yenu yenye maana. Wala msiifuatishe namna ya dunia hii; bali mgeuzwe kwa kufanywa upya nia zenu, mpate kujua hakika mapenzi ya Mungu yaliyo mema, ya kumpendeza, na ukamilifu.”        

 

Mathayo 6:19-21 “Msijiwekee hazina duniani, nondo na kutu viharibupo, na wevi huvunja na kuiba; bali jiwekeeni hazina mbinguni, kusikoharibika kitu kwa nondo wala kutu, wala wevi hawavunji wala hawaibi; kwa kuwa hazina yako ilipo, ndipo utakapokuwapo na moyo wako.”              

 

Hitimisho

Maisha ya Yakobo yanatufundisha kuwa safari ya maisha yetu duniani inaweza kugubikwa na changamoto nyingi sana lakini hata hivyo, Bado Mungu atakuwa pamoja nasi, kwa msingi huo sisi kama wakristo hatupaswi kujisahau  na badala yake tuendelee kutumaini na kuwa na imani, uvumilivu, saburi na kuwa tayari kuongozwa na Mungu na neno lake ili kufikia malengo ya kuwa pamoja naye mbinguni, na hata kama maisha yatajaa taabu kama yale ya Yakobo, Neno la Mungu lina ahidi kuwa Mungu atakuwa pamoja nasi atatushika mkono na kututia nguvu hadi mwisho wa safari yetu, Siku za miaka ya kusafiri kwetu ni chache nazo imejaa taabu. Ilikuwa ushuhuda kwa Farao pia

Ayubu 14:1-2 “Mwanadamu aliyezaliwa na mwanamke Siku zake za kuishi si nyingi, naye hujaa taabu. Yeye huchanua kama vile ua, kisha hukatwa; Hukimbia kama kivuli, wala hakai kamwe.”

Isaya 41:8-10 “Nawe, Israeli, mtumishi wangu; Yakobo, niliyekuchagua; mzao wa Ibrahimu, rafiki yangu; wewe niliyekushika toka miisho ya dunia, na kukuita toka pembe zake, nikikuambia, Wewe u mtumishi wangu; nimekuchagua wala sikukutupa; usiogope, kwa maana mimi ni pamoja nawe; usifadhaike, kwa maana mimi ni Muungu wako; nitakutia nguvu, naam, nitakusaidia, naam, nitakushika kwa mkono wa kuume wa haki yangu.”

Na. Rev. Innocent Samuel Kamote

Mkuu wa wajenzi Mwenye Hekima!.

Hakuna maoni: