Ijumaa, 4 Aprili 2025

Nendeni mkamweleze Yohana hayo mliyoyaona na kuyasikia!

 

Luka 7:19-23 “Ndipo Yohana alipowaita wawili katika wanafunzi wake, akawatuma kwa Yesu akiuliza, Wewe ndiwe yule ajaye, au tumtazamie mwingine? Nao walipofika kwake, walisema, Yohana Mbatizaji ametutuma kwako, akisema, Wewe ndiwe yule ajaye, au tumtazamie mwingine? Na saa ile ile aliwaponya wengi magonjwa yao, na misiba, na pepo wabaya; na vipofu wengi aliwakirimia kuona. Ndipo alipojibu, akawaambia, Nendeni mkamweleze Yohana hayo mliyoyaona na kuyasikia; vipofu wanapata kuona, viwete wanatembea, wenye ukoma wanatakasika, viziwi wanasikia, wafu wanafufuliwa, maskini wanahubiriwa habari njema. Naye heri mtu ye yote asiyechukizwa nami.”



Utangulizi:

Ni muhimu kufahamu kuwa katika ulimwengu tulio nao wakati mwingine wako watu ambao wangependa kujua uko wapi na unafanya nini na ni kitu gani kinaendelea katika maisha yako, wakati wote watu hao watataka kujua unaendeleaje, unafanya nini sasa na mbona siku hizi uko kimya, wao ni kama hawana kazi nyingine lakini kazi yao ni kufuatilia tu maisha ya watu na kutaka kujua uko wapi na unafanya nini na nini kinaendelea katika maisha yako, watu hawa ni kama wasoma nyota tu, wana yao lakini wanataka kujua habari zako, watataka kujua kama nyumba yako uliyojenga umemuachia nani, watataka kujua una gari? Watataka kujua una watoto wangapi? Wanataka kujua mwanao yuko wapi na anasoma shule gani, wanataka kujua hali ya mkeo ikoje, wanataka kujua hata habari za rafiki zako fulani yuko wapi? Je mmewasiliana? Yaani wao ni kutaka kufahamu tu kuwa unaendeleaje? Na kupeleleza kila kinachoendelea katika maisha yako! Sijui kama umewahi kubaini wako watu wa namna hii!. Leo tutachukua Muda kujifunza namna ya kuwajibu watu hao kutoka kwa Yesu Kristo mwenyewe, kuna namna Yesu anatufundisha nzuri sana ya kuwajibu wambeya na wapelelezi wanaotaka kujua maisha yako yanaendeleaje! Katika kifungu cha maandiko Luka 7:21-23 Yesu anaufunua moyo wake akionyesha asili yake Yeye ni nani na ametumwa kufanya nini, “He was a man in mission” Yesu alikuwa ni mtu wa kazi, kuna shughuli aliyokuwa ameandikiwa kuja kuifanya na alikuwa akiifanya kwa uaminifu, Maandiko yanaonyesha wazi na mara kadhaa Yesu aliweka wazi kuwa alikuja kufanya nini “He was an man with his assignment” alikuwa ni mtu mwenye shughuli zake!

-          Kutangaza habari njema na kuweka huru walioonewa Luka 4:18-19 “Roho wa Bwana yu juu yangu, Kwa maana amenitia mafuta kuwahubiri maskini habari njema. Amenituma kuwatangazia wafungwa kufunguliwa kwao, Na vipofu kupata kuona tena, Kuwaacha huru waliosetwa, Na kutangaza mwaka wa Bwana uliokubaliwa.”

 

-          Kutafuta na kuokoa kile kilichopotea Luka 19:10 “Kwa kuwa Mwana wa Adamu alikuja kutafuta na kuokoa kile kilichopotea.”

 

-          Kuwa fidia ya wengi kwaajili ya ukombozi wa mwanadamu Marko 10:45 “Kwa maana Mwana wa Adamu naye hakuja kutumikiwa, bali kutumika, na kutoa nafsi yake iwe fidia ya wengi.”

 

-          Kuishuhudia kweli Yohana 18:37 “Basi Pilato akamwambia, Wewe u mfalme basi? Yesu akajibu, Wewe wasema, kwa kuwa mimi ni mfalme. Mimi nimezaliwa kwa ajili ya haya, na kwa ajili ya haya mimi nalikuja ulimwenguni, ili niishuhudie kweli. Kila aliye wa hiyo kweli hunisikia sauti yangu.”

 

-          Kuwafanya mataifa yote kuwa wanafunzi Mathayo 28:18-20. “Yesu akaja kwao, akasema nao, akawaambia, Nimepewa mamlaka yote mbinguni na duniani. Basi, enendeni, mkawafanye mataifa yote kuwa wanafunzi, mkiwabatiza kwa jina la Baba, na Mwana, na Roho Mtakatifu; na kuwafundisha kuyashika yote niliyowaamuru ninyi; na tazama, mimi nipo pamoja nanyi siku zote, hata ukamilifu wa dahari.”

Kupitia maandiko hayo tunaweza kuelewa kuwa Yesu alikuwa anajitambua yeye ni nani, na yuko duniani kwaajili ya nini na kwa kweli alikuwa akitekeleza lile ambalo kwaajili ya hilo alizaliwa, unapouliza swali kuhusu maisha ya mtu anayejitambua kama ilivyo kwa Yesu Kristo basi ni vema utarajie majibu mazuri kama aliyoyapata Yohana Mbatizaji alipotaka kujua kama Yesu ndiye yule ajae au tumtazamie mwingine?  Tutajifunza somo hili Nendeni mkamweleze Yohana hayo mliyoyaona na kuyasikia kwa kuzingatia vipengele viwili vifuatavyo:-


·         Wewe ndiwe yule ajaye, au tumtazamie mwingine?    

·         Nendeni mkamweleze Yohana hayo mliyoyaona na kuyasikia


Wewe ndiwe yule ajaye au tumtazamie mwingine?

Ni muhimu kufahamu kuwa Yohana Mbatizaji alikuwa amewekwa kizuizini yaani gerezani tena kwa uonevu tu katika taabu zake na mashaka yake ya kuwekwa kizuizini huku akiwa na hofu kama haki itatendeka au la anapatwa na mashaka sio ya kuhusu maisha yake na kufungwa kwake tu bali hata kuhusu Yesu Kristo kama ni Masihi halisi au la?  Yohana ndiye aliyemtangaza Yesu Kristo wazi na kwa ujasiri kwa jamii na kuielezea jamii ya kuwa Yeye ajaye Nyuma yangu ana nguvu kuliko mimi naye atawabatiza kwa Roho Mtakatifu na kwa moto.

Mathayo 3:11 “Kweli mimi nawabatiza kwa maji kwa ajili ya toba; bali yeye ajaye nyuma yangu ana nguvu kuliko mimi, wala sistahili hata kuvichukua viatu vyake; yeye atawabatiza kwa Roho Mtakatifu na kwa moto.”

Lakini sasa akiwa gerezani Yoahana anawatuma wanafunzi wake wakaulize kwa Yesu kama kweli yeye ndiye yule ajaye au tumtazamie mwingine?  Swali hili linaonyesha mashaka aliyokuwa nayo Yohana na matatizo aliyokuwa nayo kwenye kichwa chake alipokuwa gerezani, pia swali linaonyesha kuwa Yohana naye hakuwa ameifahamu vema huduma ya Kimasihi kwa wakati ule Yeye alikuwa akimtarajia masihi ambaye atakuwa na nguvu kubwa sana za kisiasa na kijamii na kama masihi ambaye angeleta mapinduzi makubwa  ya kikoloni na kuwaondoa warumi na utawala wao na Israel kupata uhuru wa kweli kutoka kwa wakoloni hao, kama huduma hii ya kimasihi ingelikuwa ya namna hiyo hata Yeye Yohana mbatizaji angeliweza kuwekwa huru kutoka katika magereza iliyokuwa ikimkabili na mauti penginepo iliyokuwa ikimnyemelea. Yohana alikuwa ameingia shaka kama kweli unabii uliosemwa katika maandiko kumuhusu Masihi ulikuwa ndio huu, kwa maana nyingine alikuwa na mashaka na huduma aliyokuwa akiifanya Yesu Kristo kama ilikuwa huduma sahihi au la? Yeye alikuwa anaona mbona huyu jamaa yuko kimya niko gerezani mbona hafanyi kitu anachopaswa kukifanya?  Kwa hiyo alipata mashaka kuhusu utendaji wa kimasihi!

Luka 7:21-20 “Ndipo Yohana alipowaita wawili katika wanafunzi wake, akawatuma kwa Yesu akiuliza, Wewe ndiwe yule ajaye, au tumtazamie mwingine? Nao walipofika kwake, walisema, Yohana Mbatizaji ametutuma kwako, akisema, Wewe ndiwe yule ajaye, au tumtazamie mwingine?

Swali hili lenye utata linajibiwa na jibu lenye utata la Yesu Kristo ambalo kimsingi lina mambo ya kutufunza leo.

Nendeni mkamweleze Yohana hayo mliyoyaona na kuyasikia

Jibu la Yesu Kristo kwa wanafunzi wa Yohana na Yohana mwenyewe halikuwa la moja kwa moja  Ndio au hapana  na badala ayake kwanza walimkuta akiendelea na kazi ambayo kazi yenyewe ilikuwa ndio ushahidi wa nini Yesu amekuja kukifanya, Yesu kabla ya kujibu swali hilo kwanza alikuwa “busy” BIZE akishughulika na kuhubiri injili, kufundisha lakini kama haitoshi

-          Aliwafungua vipofu na wengi wakafunguliwa na kuona hapo hapo

-          Aliwafungua wenye ulemavu na wengi walitembea hapo hapo

-          Alitakasa wenye ukoma na wengi walitakasika hapo hapo

-          Aliwafungua waliokuwa viziwi na wengi walipata kusikia hapo hapo

-          Alifufua wafu na wengi walioonekana  na Misiba ilikomeshwa, pepo walikemewa na kutoka  na wagonjwa wengi sana walipokea uponyaji wao

-          Alihubiria masikini habari njema na wengi waliipokea injili

Baada ya kazi hii kubwa aliyoifanya Yesu na wanafuzi wa Yohana Mbatizaji waliishuhudia, kwa macho yao yeye mwenyewe ndipo akajibu kwa kuwaambia Nendeni mkamweleze Yohana hayo mliyoyaona na kuyasikia.

Luka 7:21-23 “Na saa ile ile aliwaponya wengi magonjwa yao, na misiba, na pepo wabaya; na vipofu wengi aliwakirimia kuona. Ndipo alipojibu, akawaambia, Nendeni mkamweleze Yohana hayo mliyoyaona na kuyasikia; vipofu wanapata kuona, viwete wanatembea, wenye ukoma wanatakasika, viziwi wanasikia, wafu wanafufuliwa, maskini wanahubiriwa habari njema. Naye heri mtu ye yote asiyechukizwa nami.”

Swali kubwa la kujiuliza hapa ni kwa nini Yesu alijibu swali la Yohana mbatizaji katika njia aliyoitumia?  Na ya wazi?

1.       Wajibu watu kivitendo – Siku zote watu wanapoingia mashaka na wewe hupaswi kwa namna yoyote ile kujitetea lakini matendo yako na misheni yako uliyopewa na Mungu itajibu kivitendo kwamba wewe ni mtu wa namna gani, Huduma ya kimasihi ilikuwa imefunikwa na utendaji mkubwa wa kimiujiza na uwezo wake wa kuwahurumia watu na kuwafungua kutoka katika vifungo vyao na mateso yao na misiba yao, kimsingi Yesu alikuwa akiutimiza unabii kwa huduma yake vile vile kama manabii walivyokuwa wametabiri na kupitia kazi alizikuwa akizifanya ilikuwa ni udhihirisho wa wazi kuwa alikuwa ni mtu na shughuli zake.

 

Isaya 61:1-2 “Roho ya Bwana MUNGU i juu yangu; kwa sababu Bwana amenitia mafuta niwahubiri wanyenyekevu habari njema; amenituma ili kuwaganga waliovunjika moyo, kuwatangazia mateka uhuru wao, na hao waliofungwa habari za kufunguliwa kwao. Kutangaza mwaka wa Bwana uliokubaliwa, na siku ya kisasi cha Mungu wetu; kuwafariji wote waliao;”

 

Yohana 5:36 “Lakini ushuhuda nilio nao mimi ni mkubwa kuliko ule wa Yohana; kwa kuwa zile kazi alizonipa Baba ili nizimalize, kazi hizo zenyewe ninazozitenda, zanishuhudia ya kwamba Baba amenituma.”

 

Yohana 10:37-38 “Kama sizitendi kazi za Baba yangu, msiniamini; lakini nikizitenda, ijapokuwa hamniamini mimi, ziaminini zile kazi; mpate kujua na kufahamu ya kuwa Baba yu ndani yangu, nami ni ndani ya Baba.”

 

Yesu anatufundisha kuwa ni kwa kufanya kazi na kwa kuonyesha kazi zetu tuzifanyazo tutathibitika kwamba tunayatimiza mapenzi ya Mungu, kama mtu ana mashaka na wewe mjibu kwa kazi za Mungu unazozifanya, namna njema ya kuondoa mashaka katika huduma zetu ni kuonyesha kazi, wewe fanya kazi, ooo huyu vilienda vikarudi waambie nionyeshe kazi, kazi zetu zinatushuhudia kama sisi ni wa Mungu au la, wako watu ni hodari sana wa kuchafua wengine na ni kama wameumbwa wawe wataalamu wa kuharibia wengine maisha lakini waambie waonyeshe kazi zao ni kazi gani wanamfanyia Mungu? Wewe uchukiaye sanamu wateka mahekalu? Mungu hataangalia uso wa mwanadamu Mungu ataangalia kazi tutapimwa na kuthibitika kwa kazi, shuhuda zetu hazitegemei wanadamu zinategemea kazi, kazi itakusemea wewe ni nani, kwa hiyo watu wanapokufuata fuata waonyeshe kazi, Yesu alionyesha kazi ili kuondoa mashaka ya Yohana mbatizaji, Mbinguni tutapimwa kwa kazi fanya kazi acha kupiga domo kazi, ee huyu sijui ilikuwa hivi ikawa vile acha upuuzi onyesha kazi, Kazi ambazo wanafunzi wa Yohana waliziona yalikuwa ni majibu tosha Yesu ni nani!

 

1Wakorintho 3:13-15 “Maana siku ile itaidhihirisha, kwa kuwa yafunuliwa katika moto; na ule moto wenyewe utaijaribu kazi ya kila mtu, ni ya namna gani. Kazi ya mtu aliyoijenga juu yake ikikaa, atapata thawabu. Kazi ya mtu ikiteketea, atapata hasara; ila yeye mwenyewe ataokolewa; lakini ni kama kwa moto.”

 

Uthibitisho wetu kuwa tumeitwa na Mungu tunatembea na Mungu na tunamtumikia Mungu ni kazi, ile neema ya Mungu iliyoko juu yetu inatenda kazi na inatufanya tufanye kazi zaidi ikiwezekana kuliko wote, watu watajaribu sana kukufanya ukose sifa kwa kukukosoa na kukuchukia na kukuuatilia Lakini ifikie wakati kila mtu aonyesha kazi, kwamba unachangia nini katika mwili wa Kristo kwa sababu kazi zetu zitapimwa, watu wengi walikuwa wakimkosoa Paulo mtume na kumuweka katika viwango vya chini na kumuona kama mtume asiye sahihi Lakini Kazi alizofanya ndio zinajibu kuwa yeye alikuwa ni Mtume wa namna gani? Watu wanaokufuata fiata waambie waangalie kazi

 

1Wakorintho 15:9-10 “Maana mimi ni mdogo katika mitume, nisiyestahili kuitwa mitume, kwa sababu naliliudhi Kanisa la Mungu. Lakini kwa neema ya Mungu nimekuwa hivi nilivyo; na neema yake iliyo kwangu ilikuwa si bure, bali nalizidi sana kufanya kazi kupita wao wote; wala si mimi, bali ni neema ya Mungu pamoja nami.”                

 

2.       Mtu asikutaabishe – Wako watu ambao ukiwa kazini wanadhani hujui unalolifanya kwa hiyo wanataka wakutaabishe, Maswali ya Yohana mbatizaji hayakumtoa Yesu Nje ya Mstari, badala yake aliendelea kuifanya kazi, kutokujibu swali la wanafuzi wa Yohana mbatizaji kwa haraka na kuanza kupiga kazi kwanza kulikuwa kunamaanisha kuwa usikubali kutaabishwa fanya kazi ile uliyoitiwa wako watu wataabishaji sana hapa duniani hawataki ufanye kile Mungu amekuitia au watataka kukubabaisha ili uondoke katika lile uliloitiwa uanze kujibizana nao, achana na magazeti ya udaku, achana na vyombo vya habari acha kujibizana na watu kwenye mitandao ya kijamii, wewe weka uso wako katika kazi, mtu anayeondoa uso wake katika kazi hafai katika ufalme wa Mungu wewe piga kazi usipoteze mwelekeo hata kidogo, Yesu alipiga kazi, kazi zitajibu

 

Luka 9:59-62 “Akamwambia mwingine, Nifuate. Akasema, Bwana, nipe ruhusa kwanza niende nikamzike baba yangu. Akamwambia Waache wafu wawazike wafu wao; bali wewe enenda ukautangaze ufalme wa Mungu. Mtu mwingine pia akamwambia, Bwana, nitakufuata; lakini, nipe ruhusa kwanza nikawaage watu wa nyumbani mwangu. Yesu akamwambia, Mtu aliyetia mkono wake kulima, kisha akaangalia nyuma, hafai kwa ufalme wa Mungu.”

 

Wagalatia 6:17 “Tangu sasa mtu asinitaabishe; kwa maana ninachukua mwilini mwangu chapa zake Yesu.”

 

Luka 13:31-32 “Saa ile ile Mafarisayo kadha wa kadha walimwendea, wakamwambia, Toka hapa, uende mahali pengine, kwa sababu Herode anataka kukuua. Akawaambia, Nendeni, mkamwambie yule mbweha, Tazama, leo na kesho natoa pepo na kuponya wagonjwa, siku ya tatu nakamilika.”

 

Mtu anayejua kusudi la Mungu, na kusudi la kuwepo kwake “a man with a mission” hawezi kutikiswa na kuacha kufanya lile aliloitiwa, Kristo Yesu kwa majibu yake kivitendo alikuwa anatukumbusha kuwa na msimamo katika shughuli zetu na wajibu wetu na yale mambo ambayo Mungu ametuitia acha kusikiliza mambo ya pembeni, pembeni wewe angalia yale ambayo ni mapenzi ya Mungu na ile kazi ambayo Mungu amekuitia kuifanya chukua chapa za Kristo, fanya kazi mtu asikutishe! Wala asikutoe nje ya mstari.

 

3.       Heri mtu yule asiye na mashaka nami - Naye heri mtu ye yote asiyechukizwa nami, Yesu alikuwa anahitimisha jibu lake kwa kutaka kumtoa shaka Yohana mbatizaji  kwamba asiye na mashaka naye wala asichukizwe naye, utendaji wake na utoaji huduma zake ulikuwa sawasawa na mapenzi ya Mungu, lakini wakati mwingine haungeweza kuwafurahisha wanadamu, kwa hiyo ingekuwa heri kama wangelikuwa na Imani naye, unapofanya lile ambalo Mungu amekuitia wakati mwingine ni vigumu kueleweka kwa ndugu zetu, jamaa zetu na hata marafiki zetu, kuna namna na jinsi ambavyo watu wanatarajia uwe na utrende katika njia wanazozifikiria wao lakini utendaji wa Mungu na mapenzi yake wakati mwingine unaweza usieleweke kwa wanadamu na ukawakwaza Yesu aliwekwa kwaajili ya kuinuka na kuanguka  wengi  katika Israel

 

Luka 2:25-34 “Na tazama, pale Yerusalemu palikuwa na mtu, jina lake Simeoni, naye ni mtu mwenye haki, mcha Mungu, akiitarajia faraja ya Israeli; na Roho Mtakatifu alikuwa juu yake. Naye alikuwa ameonywa na Roho Mtakatifu ya kwamba hataona mauti kabla ya kumwona Kristo wa Bwana. Basi akaja hekaluni ameongozwa na Roho; na wale wazazi walipomleta mtoto Yesu ndani, ili wamfanyie kama ilivyokuwa desturi ya sheria, yeye mwenyewe alimpokea mikononi mwake, akamshukuru Mungu, akisema, Sasa, Bwana, wamruhusu mtumishi wako, Kwa amani, kama ulivyosema; Kwa kuwa macho yangu yameuona wokovu wako, Uliouweka tayari machoni pa watu wote; Nuru ya kuwa mwangaza wa Mataifa, Na kuwa utukufu wa watu wako Israeli. Na babaye na mamaye walikuwa wakiyastaajabia hayo yaliyonenwa juu yake. Simeoni akawabariki, akamwambia Mariamu mama yake, Tazama, huyu amewekwa kwa kuanguka na kuinuka wengi walio katika Israeli, na kuwa ishara itakayonenewa.”

 

Huduma ya kimasihi ni yenye utata na yenye kufikirisha, na kuwakwaza wengi, utendaji wake na mafundisho yake yangeweza kusababisha mgawanyiko mkubwa na upinzani mkubwa utakaongoza wengi kujikwaa na wengi kuinuliwa katika Imani, Simeoni alimaanisha Yesu angekuwa na huduma yenye utata  na hivyo kuwa ishara itakayonenwa, Matarajio yake Yohana mbatizaji kuhusu huduma ya kimasihi kwake yangeweza kuwa kwazo kama bado angekuwa haelewi maandiko, ilikuwa ni lazima huduma ya kimasihi ilete utata miongoni mwa jamii lakini ana heri mtu yule ambaye angeamini ambaye hangekuwa na mashaka naye ambaye hatakwazwa na yeye, kukwazwa na huduma ya kimasihi ilikuwa ni jambo la kawaida na lilikuwa limetabiriwa na Isaya na pia Mzee Simeoni

 

Isaya 8:14-15 “Naye atakuwa ni mahali patakatifu; bali ni jiwe la kujikwaza na mwamba wa kujikwaa kwa nyumba za Israeli zote mbili, na mtego na tanzi kwa wenyeji wa Yerusalemu. Na wengi watajikwaa juu yake, na kuanguka na kuvunjika, na kunaswa na kukamatwa.”

 

Yesu alitaka kumsaidia Yohana Mbatizaji asiwe na mashaka naye aendelee kumuamini, hata kama Yesu hatamtoa gerezani lakini hapaswi kuchanganyikiwa kuhusu Yesu, Yesu hakutaka Yohana awe miongoni mwa wale wengi wataakaojikwaa juu yake, lakini alitaka kumpa jibu thabiti kwamba awe na imani njia za Mungu za kiutendaji ziko juu sana kuliko tunavyofikiri, usikwazike ukiona katika maisha yako ni kama Yesu hashughuliki na wewe usimlaumu wala usiwe na mashaka naye endele kupiga kazi, utendaji wa Mungu ni utendaji wa kipekee na wa ajabu na njia zake ziko tofauti na matarajio yetu na utendaji wake.

Hitimisho:

Njia za Mungu za kiutendaji sio njia zetu, utendaji wa Mungu unazidi utendaji wa fikra ya kawaida ya kibinadamu, ni lazima tuwe tayari kufuata njia na mapenzi ya Mungu, wale watu wanaotaka kujua kuwa tuko wapi tunafanya nini, tunaendeleaje, familia zetu zikoje tuna watoto wangapi, tumejenga au la, tuna mashamba au la, tuna magari au la! tuko wapi tuna ishu gani au la, tunamiliki fedha au la watu wanaofuatilia maisha yako waambie Kazi za Mungu zinaendelea, waambie unachukua chapa za Kristo waambie wasiwe na mashaka na wewe!, kuna wale waliokukwamisha pia watatamani kujua uko wapi sasa na unaendeleaje, kuna wale waliokufukuza kazi, kuna wale waliokuwekea fitina wakadhani ya kuwa utakwama, waambie waendelee kutufuatilia katika mitandao ya kijamii wapitie kurasa zetu facebook na kwenye blogu zetu waambie ya kuwa neno la Mungu linaendelea, waambie tunaendelea kuihubiri injili vile vile na hatujawahi kukaa kimya, waambie tunaendelea kufanya wanafunzi waambie kazi za Mungu zinaendelea kamakawaida, waambie watu wanaokoka, waambie tunaendelea na wokobvu na wala hatuna mpango wa kurudi nyuma,  waambie kazi zinaendelea na hakuna wa kutuzuia, pepo wanatoka, habari njema inahubiriwa, wafungwa wanafunguliwa na vipofu wanapewa kuona, Nyaraka zinaandikwa na maisha yanaendelea  heri yake mtu yule asiye na mashaka nami!, Heri yake mtu yule asioyechukizwa nami!

Rev. Innocent Samuel Kamote.

Mkuu wa wajenzi mwenye Hekima.

Maoni 1 :

Bila jina alisema ...

Ahsante mchungaji