Ijumaa, 11 Aprili 2025

Neno la Mungu halifungwi!


2Timotheo 2:8-9 “Mkumbuke Yesu Kristo, aliyefufuka katika wafu, wa uzao wa Daudi kama inenavyo injili yangu. Nami katika hiyo nimeteswa hata kufungwa kama mtenda mabaya; lakini neno la Mungu halifungwi. Kwa ajili ya hilo nastahimili mambo yote, kwa ajili ya wateule, ili wao nao waupate wokovu ule ulio katika Kristo Yesu, pamoja na utukufu wa milele.”

 


      

Utangulizi

Kauli ya kuwa Neno la Mungu halifungwi, ilitamkwa na Mtume Paulo ambaye wakati huu alikuwa kifungoni, Paulo alifungwa na kupitia mateso kwa sababu alikuwa akiihubiri injili na kufundisha watu Neno la Mungu ambalo alikuwa na Imani kwamba litawafungua watu kutoka dhambini na kuwaelimisha, Hata hivyo kutokana na njama za shetani Paulo mtume mara kadhaa aliwekwa kizuizini na kufungwa gerezani shetani akifikiri ya kuwa kwa kufanya hayo ataweza kuzia kasi ya injili na utendaji wa Roho Mtakatifu katika maisha ya muhubiri huyu Mashuhuri wa karne ya Kwanza, Hata hivyo Paulo Mtume alikuwa na ujuzi na uzoefu  ya kuwa Neno la Mungu halifungwi!, vizuizi kwa Paulo mtume kamwe havikuweza kudhoofisha Nguvu ya injili, kwani wakati mwingine aliweza kuhubiri akiwa kifungoni na kuwafikia wengi huko na zaidi ya yote alipata nafasi ya kuandika mafundisho ambayo kimsingi yaliweza kuinua kwa kiasi kikubwa maisha ya waamumini wa makanisa wa nyakati za kanisa la Kwanza hata leo, kwa hiyo tunajifunza ya kuwa licha ya mateso, vikwazo na vifungo mbali mbali ambavyo tunakutana navyo kwaajili ya injili kumbe Neno la Mungu halifungwi!

2Timotheo 2:9 “Nami katika hiyo nimeteswa hata kufungwa kama mtenda mabaya; lakini neno la Mungu halifungwi.”                

Kwa Msingi huo leo tutachukua Muda kujifunza kwa undani usemi wa Paulo kuwa neno la Mungu Halifungwi kwa kuzingatia vipengele vitatu vifuatavyo:-


·         Injili ina nguvu kuliko vifungo vya gerezani

·         Mifano ya watu waliofungwa kwaajili ya injili

·         Neno la Mungu halifungwi!

 

Injili ina nguvu kuliko vifungo vya gerezani

Wote tunafahamu kuwa habari njema za Yesu Kristo zina nguvu kubwa sana ya kuwafungua watu na kuwaweka huru kutoka katika vifungo mbalimbali vya shetani pamoja na utumwa wa dhambi, ni ukweli usiopingika kuwa injili ni uweza wa Mungu uletao wokovu, kwa kila aaminiye bila kujali anatokea katika utamaduni wa aina gani, wala bila kujali hekima au elimu aliyonayo mtu.

Warumi 1:14-16 “Nawiwa na Wayunani na wasio Wayunani, nawiwa na wenye hekima na wasio na hekima. Kwa hiyo, kwa upande wangu, mimi ni tayari kuihubiri Injili hata na kwenu ninyi mnaokaa Rumi. Kwa maana siionei haya Injili; kwa sababu ni uweza wa Mungu uuletao wokovu, kwa kila aaminiye, kwa Myahudi kwanza, na kwa Myunani pia.”

Kwa utambuzi na uzoefu wa namna Paulo alivyoona injili ikiwasaidia wengi na kuwafungua kutoka katika vifungo vya giza na dhambi, Paulo aliendelea kushikwa na shauku ya kuihubiri injili kila mahali na kila wakati, hata hivyo katika namna ya kushangaza sana Paulo mtume mara kadhaa alikamatwa na kutiwa gerezani, kama muhalifu/au mtenda mabaya kwa sababu ya injili aliyokuwa anaihubiri, Paulo alitamani sana kuwa huru ili aweze kuieneza injili, Lakini Ibilisi alikusudia kumzuia na sio tu kuwa aliwekwa gerezani lakini pia alilindwa na askari na kufungwa kwa minyororo kama moja ya wahalifu hatari sana, kwa hiyo mara nyingine aliwaandikia makanisa mbalimbali wamuombee, ili afunguliwe kinywa na kuihubiri injili kwa ujasiri mkubwa, Lakini hata hivyo alikuwa amefungwa

Waefeso 6:18-20 “kwa sala zote na maombi mkisali kila wakati katika Roho, mkikesha kwa jambo hilo na kudumu katika kuwaombea watakatifu wote; pia na kwa ajili yangu mimi, nipewe usemi kwa kufumbua kinywa changu, ili niihubiri kwa ujasiri ile siri ya Injili; ambayo kwa ajili yake mimi ni mjumbe katika minyororo; hata nipate ujasiri katika huyo kunena jinsi inipasavyo kunena.”

Katika hali ngumu kama hiyo, akiwa gerezani, na katika vifungo na chini ya mikatale akiwa mfungwa au mjumbe wa minyororo bado anawaomba kanisa kumuombea ili apewe ujasiri aendelee kulisema neno la Mungu, Paulo alifanya hivyo akiihubiri injili kwa wafalme, wafungwa na wakuu wa magereza ambao kimsingi walifunguliwa na walipata neema ya kusikia habari njema licha ya kuwa Mtumishi wa Mungu alikuwa katika minyororo, aliendelea kuhubiri kwa ujasiri mahakamani, kwa mahakimu na wasikilizaji lakini pia aliendelea kuandika nyaraka mbali mbali ambazo zilikuwa na mafundisho mazuri na ya msingi akiyatia moyo na kuwajenga wale aliokuwa amewahubiri injili pamoja na mwili wa Kristo kokote uliko ulimwenguni.

Matendo 26:27-29 “Mfalme Agripa, je! Wawaamini manabii? Najua ya kuwa wawaamini. Agripa akamwambia Paulo, Kwa maneno machache wadhani kunifanya mimi kuwa Mkristo. Paulo akamjibu, Namwomba Mungu kwamba, ikiwa kwa machache au ikiwa kwa mengi, si wewe tu ila na hao wote wanaonisikia leo wawe kama mimi, isipokuwa vifungo hivi.”

Vifungo havikumzuia Paulo Mtume kuihubiri injili, alihubiri kwa ujasiri wote, alihubiri wafalme mahakamani na wasikilizaji wa kesi wote akiendelea kuwashawishi waijuie injili na kumuamini Mwana wa Mungu, Paulo hakujali injili inahubiriwa wapi, alikuwa gerezani lakini alitamani watu wote wabadilike wawe kama yeye isipokuwa vifungo vyake tu, kwa maneno yake na matendo yake inatufundisha kuwa injili ina nguvu kuliko magereza, magereza ilikuwa shimoni, mwanga ukiwa hafifu sana lakini Moyo wa Paulo uliendelea kumuwaka akiwa na shauku ya kuisema injili, kufungwa kwake kulitumiwa na maadui kama njia ya kuhubiri kwa fitina injili isiyofaa lakini kulitumiwa na watu wazuri kuwapa ujasiri wa kuisema injili kwa nguvu kubwa huku yeye akiendelea kuandika nyaraka za kuwatia moyo makanisa mbalimbali na mwili wa Kristo.

Wafilipi 1:12-13 “Lakini, ndugu zangu, nataka mjue ya kuwa mambo yote yaliyonipata yametokea zaidi kwa kuieneza Injili; hata vifungo vyangu vimekuwa dhahiri katika Kristo, miongoni mwa askari, na kwa wengine wote pia. Na wengi wa hao ndugu walio katika Bwana, hali wakapata kuthibitika kwa ajili ya kufungwa kwangu, wamezidi sana kuthubutu kunena neno la Mungu pasipo hofu.”

Neno la Mungu limedhihirika kuwa na nguvu sana kuliko mipaka ya kibinadamu na utendaji wa shetani, Injili ina nguvu kuliko vifungo vya gerezani, ina nguvu kuliko vizuizi vya shetani, ina nguvu kuliko vifungo vya kidini, ina nguvu kuliko wivu wa wanadamu na husuda zao, injili haiwezi kuzuiwa na mtu yeyote, wala haiwezi kuziwa na vita vya kijinga vya maadui wa injili, Injili itaendelea kuhubiriwa hata kwa kalamu, itapelekwa kwa mitandao ya kijamii, itapenya kwa sauti za Redio na televisheni, hakuna dhehebu, wala dini, wala taifa, wala ufalme, wala bara, wala kisiwa ambacho kitaweza kuizuia injili, nguvu za giza haziwezi, mapepo na majini hayawezi, mila na desturi haziwezi injili ina nguvu kuliko maregeza yoyote ile, inaweza kupenya kwa askari, inaweza kupenya kwa daktari, inaweza kupenya kwa mkulima, inaweza kuwafikiwa wachimba madini, inaweza kuwafikia wanasiasa, inaweza kumfikia yeyote yule kwa njia yeyeote ile, Paulo alitumia mateso yake na vifungo vyake kumkumbusha Timotheo na kumtia moyo kwamba asiogope kwani Yesu aliteseka pia kwaajili ya injili, lakini alifufuka, hakuna mateso yanayoweza kuizuia injili, wala hila, wala vifungo neno la Mungu litaendelea mbele, wapinzani watakufa lakini neno la Mungu halifi, hivyo kila Muhubiri wa injili hapaswi kuogopa kuisema kweli ya Mungu kwa sababu watu wa Mungu watafunguliwa kwa injili ya kweli na sio injili ya hila na uongo hubiri kweli saidia watu kuwa huru na unaweza kwa injili.

Mifano ya watu waliofungwa kwaajili ya injili

Ni muhimu kufahamu kuwa tunapaswa kuihubiri injili katika mazingira yoyote yale yawe magumu yawe laini, bila kujali kwamba kuna vikwazo vya aina gani, kumbuka kuwa kwa kadiri siku zinavyokwenda mbele upinzani wa kiinjili unaendelea kuchukua sura mpya, shetani sasa anaweza kuwatumia viongozi wa kidini na kidhehebu kuhakikisha kuwa wanakuziba kinywa ili usihubiri injili, kumbuka tu kuwa watakatifu waliotutangulia wote waliopewa maagizo ya neno la Mungu walipitishwa katika nyakati ngumu na kufungwa na kuzibwa vinywa vyao kwaajili ya injili hata hivyo bado tunaonyeshwa ya kuwa neno lilisimama na wale waliokuwa huru waliisema injili kila mahali.

1.       Paulo na Sila walipokuwa wakiihubiri injili ambayo ilifungua watu na zaidi sana mwanamke mwenye pepo wa uaguzi, mji ulitaharuki, wakafanyiwa ghasia, wakapelekwa mahakamani, wakisingiziwa kesi ya kuchafua mji, wakavuliwa nguo, wakapigwa kwa bakora, wakatupwa gerezani wakafungwa miguu yao kwa mikatale wakiwa wamepokea mapigo mengi, hawakuweza kutulia walipokuwa ndani gerezani wakifungwa kama wahalifu hawakukata tamaa, wala hawakunyamaza, waliendelea kuisema injili walimwimbia Mungu na kuomba usiku kucha, Na Mungu akatuma tetemeko kubwa gereza na vifungo vyote vya watu wote vikaaachia na hatimaye mkuu wa gereza na nyumba yake wakaokoka, shetani kwa ujinga wake alifikiri kwa kumuweka Paulo na sila kizuizini ataizuia injili na badala yake injili iliwafikiwa wafungwa wote na mkuu wa gereza na familia yake wote waliokoka na kubatizwa

 

Matendo 16:19-34 “Basi bwana zake walipoona ya kuwa tumaini la faida yao limewapotea, wakawakamata Paulo na Sila, wakawakokota mpaka sokoni mbele ya wakuu wa mji; wakawachukua kwa makadhi, wakasema, Watu hawa wanachafua sana mji wetu, nao ni Wayahudi; tena wanatangaza habari ya desturi zisizokuwa halali kwetu kuzipokea wala kuzifuata, kwa kuwa sisi tu Warumi. Makutano wote wakaondoka wakawaendea, makadhi wakawavua nguo zao kwa nguvu, wakatoa amri wapigwe kwa bakora. Na walipokwisha kuwapiga mapigo mengi, wakawatupa gerezani, wakamwamuru mlinzi wa gereza awalinde sana. Naye akiisha kupata amri hii akawatupa katika chumba cha ndani, akawafunga miguu kwa mkatale. Lakini panapo usiku wa manane Paulo na Sila walikuwa wakimwomba Mungu na kumwimbia nyimbo za kumsifu, na wafungwa wengine walikuwa wakiwasikiliza. Ghafula pakawa tetemeko kuu la nchi, hata misingi ya gereza ikatikisika, na mara hiyo milango ikafunguka, vifungo vya wote vikalegezwa. Yule mlinzi wa gereza akaamka, naye alipoona ya kuwa milango ya gereza imefunguka, alifuta upanga, akataka kujiua, akidhani ya kuwa wafungwa wamekimbia. Ila Paulo akapaza sauti yake kwa nguvu, akisema, Usijidhuru, kwa maana sisi sote tupo hapa. Akataka taa ziletwe, akarukia ndani, akitetemeka kwa hofu, akawaangukia Paulo na Sila; kisha akawaleta nje akasema, Bwana zangu, yanipasa nifanye nini nipate kuokoka? Wakamwambia, Mwamini Bwana Yesu, nawe utaokoka pamoja na nyumba yako. Wakamwambia neno la Bwana, yeye na watu wote waliomo nyumbani mwake. Akawakaribisha saa ile ile ya usiku, akawaosha mapigo yao, kisha akabatizwa, yeye na watu wake wote wakati uo huo. Akawaleta juu nyumbani kwake, akawaandalia chakula, akafurahi sana, yeye na nyumba yake yote, maana amekwisha kumwamini Mungu.”

               

2.       Petro na Yohana  - Waliwekwa gerezani na wakuu wa makuhani na masadukayo kwaajili ya wivu walipokuwa wakiihubiri injili na kuijaza Yerusalemu mafundisho yao, wakuu wa makuhani na wazee wa dini waliwakataza wasihubiri kwa jina la Yesu wala nguvu zake za ufufuo na kuamua kuwaweka gerezani, lakini malaika wa Bwana alikuja kwa muujiza na kuwafungua na kuwaagiza tena wakaseme habari njema na kuendelea kuwafundisha watu

 

Matendo 4:1-20 “Hata walipokuwa wakisema na watu wale, makuhani na akida wa hekalu na Masadukayo wakawatokea, wakifadhaika sana kwa sababu wanawafundisha watu na kuhubiri katika Yesu ufufuo wa wafu. Wakawakamata, wakawaweka gerezani hata asubuhi; kwa kuwa imekwisha kuwa jioni. Lakini wengi katika hao waliosikia lile neno waliamini; na hesabu ya watu waume ikawa kama elfu tano. Hata asubuhi wakubwa na wazee na waandishi wakakusanyika Yerusalemu, na Anasi Kuhani Mkuu, na Kayafa pia, na Yohana na Iskanda, na wote wale waliokuwa jamaa zake Kuhani Mkuu. Walipowaweka katikati wakawauliza, Kwa nguvu gani na kwa jina la nani ninyi mmefanya haya? Ndipo Petro, akijaa Roho Mtakatifu, akawaambia, Enyi wakubwa wa watu na wazee wa Israeli, kama tukiulizwa leo habari ya jambo jema alilofanyiwa yule mtu dhaifu, jinsi alivyoponywa, jueni ninyi nyote na watu wote wa Israeli ya kuwa kwa jina la Yesu Kristo wa Nazareti, ambaye ninyi mlimsulibisha, na Mungu akamfufua katika wafu, kwa jina hilo mtu huyu anasimama ali mzima mbele yenu. Yeye ndiye jiwe lile lililodharauliwa na ninyi waashi, nalo limewekwa kuwa jiwe kuu la pembeni. Wala hakuna wokovu katika mwingine awaye yote, kwa maana hapana jina jingine chini ya mbingu walilopewa wanadamu litupasalo sisi kuokolewa kwalo. Basi walipoona ujasiri wa Petro na Yohana, na kuwajua ya kuwa ni watu wasio na elimu, wasio na maarifa, wakastaajabu, wakawatambua ya kwamba walikuwa pamoja na Yesu. Na wakimwona yule aliyeponywa akisimama pamoja nao hawakuwa na neno la kujibu. Wakawaamuru kutoka katika baraza, wakafanya shauri wao kwa wao, wakisema, Tuwafanyie nini watu hawa? Maana ni dhahiri kwa watu wote wakaao Yerusalemu ya kwamba ishara mashuhuri imefanywa nao, wala hatuwezi kuikana. Lakini neno hili lisije likaenea katika watu, na tuwatishe wasiseme tena na mtu awaye yote kwa jina hili. Wakawaita, wakawaamuru wasiseme kabisa wala kufundisha kwa jina la Yesu. Petro na Yohana wakawajibu wakawaambia, Kwamba ni haki mbele za Mungu kuwasikiliza ninyi kuliko Mungu, hukumuni ninyi wenyewe; maana sisi hatuwezi kuacha kuyanena mambo tuliyoyaona na kuyasikia.

 

Matendo 5:18-25 “wakawakamata mitume wakawaweka ndani ya gereza; lakini malaika wa Bwana akafungua milango ya gereza usiku, akawatoa, akasema, Enendeni mkasimame hekaluni mkawaambie watu maneno yote ya Uzima huu. Nao waliposikia wakaenda alfajiri hekaluni, wakaanza kufundisha. Akaja Kuhani Mkuu nao waliokuwa pamoja naye, wakawakutanisha watu wa baraza, na wazee wote wa wana wa Israeli, wakatuma watu gerezani ili wawalete. Hata watumishi walipofika hawakuwaona gerezani, wakarudi wakatoa habari, wakisema, Gereza tumeikuta imefungwa salama, nao walinzi wamesimama mbele ya mlango; lakini tulipoufungua hatukukuta mtu ndani. Basi jemadari wa hekalu na wakuu wa makuhani waliposikia haya, wakaingiwa na shaka kwa ajili yao, litakuwaje jambo hilo. Mtu mmoja akaja akawapasha habari ya kwamba, Watu wale mliowaweka gerezani wako ndani ya hekalu, wamesimama wakiwafundisha watu.

 

3.       Yeremia nabii alifungwa lakini neno la Mungu lilienea - Historia na tabia ya Mungu inaonyesha ya kuwa neno lake halijawahi kufungwa wala kuwekwa kizuizini, shetani anaweza kutumia hila kuwatesa na kuwaweka kizuizini watumishi wa Mungu lakini Historia inamuhukumu kuwa hajawahi weza kushidana na Roho wa Mungu na Hekima aliyo nayo Mungu katika kuyahifadhi mapenzi yake, Yeremia yeye alitiwa Gerezani kwa sababu ya kuwaonya watu kuhusu kuharibiwa kwa Yerusalem na hekalu pia, lakini pamoja na kufungwa aliendelea kupenyeza ujumbe wa Mungu kwa mfalme na unabii wa ujumbe wa Mungu kwa watu wake uliendelea

 

Yeremia 37:15-17 “Nao wakuu wakamkasirikia Yeremia, wakampiga, wakamtia gerezani katika nyumba ya Yonathani, mwandishi; kwa maana ndiyo waliyoifanya kuwa gereza. Basi, Yeremia alipokuwa ameingia katika nyumba ya shimo, na katika vyumba vya ndani; na Yeremia alipokuwa amekaa humo siku nyingi; ndipo Sedekia, mfalme, akatuma watu wamlete; naye mfalme akamwuliza kwa siri ndani ya nyumba yake, akasema, Je! Liko neno lililotoka kwa Bwana? Yeremia akasema, Liko. Akasema pia, Utatiwa katika mikono ya mfalme wa Babeli.”               

 

4.       Yesu Kristo aliuawa kwaajili ya injili – Wakuu wa dini na makuhani walipanga njama za kummaliza Yesu, walifikiri kwa ufupi ya kuwa wakimmaliza basi watakuwa wameondoa ujumbe wake na kupunguza kadhia ya kusikia Yesu akiwa maarufu siku hadi siku, walimsingizia mengi, walimtesa, aliteswa sana alipigwa mijeledi mikali, walimdhihaki na kumsulubisha msalabani, hawakujua ya kuwa huo ndio ulikuwa mwanzo wa mapinduzi makubwa ya kiinjili, Mwanaume huyu mmbora alifufuka siku ya tatu na habari zake zilihubiriwa mpaka leo na yeye ameamuru habari hizi na mafundisho yake yahubiriwe na kufundishwa kwa wanafunzi wa mataifa yote

 

1Wakorintho 2:6-8. “Walakini iko hekima tusemayo kati ya wakamilifu; ila si hekima ya dunia hii, wala ya hao wanaoitawala dunia hii, wanaobatilika; bali twanena hekima ya Mungu katika siri, ile hekima iliyofichwa, ambayo Mungu aliiazimu tangu milele, kwa utukufu wetu; ambayo wenye kuitawala dunia hii hawaijui hata mmoja; maana kama wangaliijua, wasingalimsulibisha Bwana wa utukufu;

 

Mathayo 28:18-20 “Yesu akaja kwao, akasema nao, akawaambia, Nimepewa mamlaka yote mbinguni na duniani. Basi, enendeni, mkawafanye mataifa yote kuwa wanafunzi, mkiwabatiza kwa jina la Baba, na Mwana, na Roho Mtakatifu; na kuwafundisha kuyashika yote niliyowaamuru ninyi; na tazama, mimi nipo pamoja nanyi siku zote, hata ukamilifu wa dahari.

 

Yohana 12:24 “Amin, amin, nawaambia, Chembe ya ngano isipoanguka katika nchi, ikafa, hukaa hali iyo hiyo peke yake; bali ikifa, hutoa mazao mengi.   

 

Kifo cha Yesu Kristo cha mateso, kileleta ukombozi mkubwa sana kwa wanadamu na kusababisha neno la Mungu kuenea kwa kasi kubwa duniani, tunajifunza hapa kuwa neno la Mungu sio tu kuwa halifungwi lakini halizikwi, ni kukosa hekima na ni ujinga mkubwa kujaribu kuizuia injili kwa sababu zozote zile, kila wakati shetani anapojaribu kuleta vikwazo kuizuia injili anakuwa kama mtu anayechochea moto na kusababisha chakula kiive haraka, upinzani mkubwa ulisababisha kazi kubwa na ueneaji mkubwa wa injili, Ndugu haijalishi wanaoizuia injili ni makuhani, au wakuuwa dini au mafarisayo au masadukayo au wanasiasa vyovyote iwavyo Neno la Mungu litaendelea  na hakuna mwanadamu anayeweza kizuia injili. Mtu akiifunga injili malaika wa Bwana watakunong’oneza kwa kukuambia Enendeni mkasimame mkawaambie watu maneno yote ya uzima huu!

 

Matendo 5: 18-21bwakawakamata mitume wakawaweka ndani ya gereza; lakini malaika wa Bwana akafungua milango ya gereza usiku, akawatoa, akasema, Enendeni mkasimame hekaluni mkawaambie watu maneno yote ya Uzima huu. Nao waliposikia wakaenda alfajiri hekaluni, wakaanza kufundisha

Neno la Mungu halifungwi!

Tumeona na sasa unaweza kukubaliana na ukweli wa maneno ya Paulo mtume ya kuwa neno la Mungu halifungwi, Katika historia nzima ya dunia tumeona shetani akiwatumia watu na wafalme na mataifa mbalimbali kuzizuia habari za Yesu, lakini pia madhehebu na viongozi wa dini wakiwa sababu ya kuizuia injili lakini daima shetani na maajenti wake wote wamethibitisha kufeli, usikubali kupoa, usikubali moto wa injili uzimike katika maisha yako, ni lazima tuhakikishe ya kuwa tunakirithisha kijiti hiki au mwenge huu au nuru hii kwa kizazi kingine waipeleke injili bila kujali vikwazo wanavyokutana navyo, Mateso, upinzani na vifungo kamwe havijawahi kuwa sababu ya kuizuia injili na badala yake kama upinzani wa upepo kwa ndege inayotaka kupaa ndio ulivyo upinzani wa injili husababisha moto uwake na kukolea zaidi.

2Timotheo 2:8-9 “Mkumbuke Yesu Kristo, aliyefufuka katika wafu, wa uzao wa Daudi kama inenavyo injili yangu. Nami katika hiyo nimeteswa hata kufungwa kama mtenda mabaya; lakini neno la Mungu halifungwi. Kwa ajili ya hilo nastahimili mambo yote, kwa ajili ya wateule, ili wao nao waupate wokovu ule ulio katika Kristo Yesu, pamoja na utukufu wa milele.”

Tunao ushuhuda ya kuwa mataifa mengi, wafalme wengi na wenye mamlaka wengi wamejaribu kuipinga injili lakini injili imeenea kila mahali ulimwenguni, yako maeneo ambayo Biblia imepigwa marufuku lakini uthibitisho tulio nao leo duniani ni kuwa bado ndicho kitabu kinachoongozwa kwa kusomwa zaidi duniani, Yako makanisa yamefungwa na wako wakristo ambao wako katika mateso ya aina mbalimbali, lakini hayo hajayasaidia kuifanya injili isisonge mbele, wewe nawe mtu wa Mungu unaweza kuwa unapitia vikwazo vya namna mbalimbali, wakuu wa dini wanakukandamizia, hawataki uibuke, wanataka upotee kwa sababu una mafundisho sahihi, una injili iliyo sahihi wewe bado ni wa moto nataka kukutia moyo ya kuwa unayoyapitia hayawezi kukufanya unyamaze neno la Mungu litaendelea  kila kitu duniani kitapia lakini maneno ya Mungu hayatapita kamwe, Kama makusudi ya Mungu hayawezi kuzuilika kumbuka ya kuwa kusudi kubwa la Mungu ni injili hakuna mtu anayeweza kuizuia injili lihubiri neno bila kujali wakati unaofaa na wakati usiofaa hubiri neno!

Isaya 40:7-8 “Majani yakauka, ua lanyauka; Kwa sababu pumzi ya Bwana yapita juu yake. Yakini watu hawa ni majani. Majani yakauka, ua lanyauka; Bali neno la Mungu wetu litasimama milele.”

Hitimisho;
Neno la Mungu halifungwi, Paulo mtume alikuwa na ufahamu huo ya kwamba hata ingawa yeye yuko kifungoni, hekima ya shetani imeshindwa kwa hekima ya Mungu, shetani hakuweza kuzuia kabisa ujumbe wa kitume usiwafikie watu, watu hawakuweza kuisikia sauti yake lakini mafundisho yenye uzima yaliwafikiwa watu kupitia nyaraka zake, hakuna mwanadamu anayeweza kulifunga neno la Mungu na kufanya hivyo ni upuuzi na hekina ya kibinadamu na ya shetani, Shetani hawezi kuzuia mpango wa Mungu, kila wakati mipango ya giza imehibitisha kufeli vibaya, mateso na vifungo havujawahi kuwa mwisho wa kazi ya Mungu, badala yake imekuwa njia ya kuonyesha utukufu wake na nguvu,  injili itaendelea kuhubiriwa na kufundishwa pasipo hofu hata kama tutakutana na vikwazo, Mungu atafanya kila njia ili kwamba neno lake lizidi kukua  na kuenea Je umekuwa unakabiliwa na hofu kama Timotheo kwaajili ya vikwazo? Usiogope neno la Mungu halifungwi!

Marko 13:31 “Mbingu na nchi zitapita; lakini maneno yangu hayatapita kamwe.”

 

Na. Rev. Innocent Samuel Kamote

Mkuu wa wajenzi mwenye hekima!

Hakuna maoni: