Mathayo 2:19-21 “Hata alipofariki Herode,
tazama, malaika wa Bwana alimtokea Yusufu katika ndoto huko Misri, akasema,
Ondoka, umchukue mtoto na mamaye, ushike njia kwenda nchi ya Israeli; kwa maana
wamekufa walioitafuta roho ya mtoto. Akaondoka akamchukua mtoto na mamaye,
akafika nchi ya Israeli.”
Utangulizi:
Malaika wa Bwana alimwambia
Yusufu maneno haya alipokuwa akali akiishi Misri, mahali alikokuwa ameelekezwa
kwaajili ya kwenda kumficha mtoto Yesu baada ya kutafutwa kuuawa na Mfalme
Herode mkuu, kwa hofu ya kutokutaka kuwepo kwa mfalme mpya wa Wayahudi, tabia
ya Herode ilikuwa ni matokeo ya wivu wake na mpango wa kishetani wa kutaka
kuharibu mpango na mapenzi ya Mungu kwaajili ya ukombozi wa mwanadamu kwa
kutaka kumuua Yesu. Somo hili ni maonyo kwa watu wote wasio na mapenzi mema kwa
kazi na mpango wowote wa Mungu, Mungu yuko tayari kuulinda mpango wake na
makusudi yake kwa gharama yoyote ile, na hakuna mtu awaye yote anayeweza kuwa
bora kuliko mpango na makusudi ya Mungu!
Mathayo 2:13 – 14 “Na hao walipokwisha
kwenda zao, tazama, malaika wa Bwana alimtokea Yusufu katika ndoto, akasema,
Ondoka, umchukue mtoto na mama yake, ukimbilie Misri, ukae huko hata nikuambie;
kwa maana Herode anataka kumtafuta mtoto amwangamize. Akaondoka akamchukua
mtoto na mama yake usiku, akaenda zake Misri;”
Herode ambaye alitafuta kumuangamiza
Yesu alikuwa amekwishakufa, Yesu alipaswa kukulia Nazareth katika inchi ya
Israel inchi ya utumishi wake na aliyekuwa kipingamizi cha mpango huo alikuwa
ameondolewa na Bwana mwenyewe hivyo Kristo angetekeleza mapenzi ya Mungu bila
kizuizi, katika inchi ya Israel kwa sababu hiyo sasa malaika wa Bwana anatoa
wito wa wao kurejea huku akiweka bayana sababu za kurejea ni kuwa wamekufa
waliokuwa wakiitafuta roho ya mtoto!
Mathayo 2:22-23 “Lakini aliposikia ya
kwamba Arkelao anamiliki huko Uyahudi mahali pa Herode babaye, aliogopa kwenda
huko; naye akiisha kuonywa katika ndoto, akasafiri pande za Galilaya, akaenda,
akakaa katika mji ulioitwa Nazareti; ili litimie neno lililonenwa na manabii,
Ataitwa Mnazorayo.”
Tutajifunza somo hili “Kwa maana
wamekufa waliokuwa wakiitafuta roho ya mtoto” kwa kuzingatia vipengele viwili
vifuatavyo:-
·
Hatari ya
kuzuia mpango wa Mungu.
·
Kwa maana
wamekufa waliokuwa wakiitafuta roho ya Mtoto.
Hatari ya kuzuia mpango wa Mungu
Ni muhimu kufahamu kuwa hakuna
jambo baya na la hatari sana duniani kama kujaribu kuzuia mapenzi ya Mungu au
Mpango wa Mungu, mtu awaye yote wa mamlaka ya aina yoyote ile ambaye atasimama
kuzuia kusudi la Mungu au kujaribu kusimamisha mpango wa Mungu juu ya kile
alichokikusudia Mungu anajiweka katika hatari isiyoweza kusimulika, kuzuia
makusudi ya Mungu wakati wowote na kwa sababu zozote zile ni kuingia katika
mfumo wa Mungu. Mfalme Herode mkuu kwa ujumla hakufurahia taarifa za kuzaliwa
kwa Masihi ambaye kimsingi ni mfalme wa wayahudi, na badala yake alianza
mipango mikakati ya kutaka kumuua Yesu na kuharibu mpango wa Mungu wa ukombozi
kwa mwanadamu, Kiburi cha kibinadamu na ulevi wa madaraka ulimfanya mfalme huyu
mjinga kujifikiri ya kuwa yeye ni Muhimu kuliko mpango wa Mungu, na kwa akili
zake ndogo alifanikiwa kusababisha misiba kwa wamama wa Bethelehemu waliokuwa
na watoto wadogo chini ya miaka miwili.
Mathayo 2:3-8 “Basi mfalme Herode
aliposikia hayo, alifadhaika, na Yerusalemu pia pamoja naye. Akakusanya wakuu
wa makuhani wote na waandishi wa watu, akatafuta habari kwao, Kristo azaliwa
wapi? Nao wakamwambia, Katika Bethlehemu ya Uyahudi; kwa maana ndivyo
ilivyoandikwa na nabii, Nawe Bethlehemu, katika nchi ya Yuda, Hu mdogo kamwe
katika majumbe wa Yuda; Kwa kuwa kwako atatoka mtawala Atakayewachunga watu
wangu Israeli. Kisha Herode akawaita wale mamajusi faraghani, akapata kwao
hakika ya muda tangu ilipoonekana ile nyota. Akawapeleka Bethlehemu, akasema,
Shikeni njia, mkaulize sana mambo ya mtoto; na mkiisha kumwona, nileteeni
habari, ili mimi nami niende nimsujudie.”
Mathayo 2:16-18 “Ndipo Herode, alipoona ya
kuwa amedhihakiwa na wale mamajusi, alighadhabika sana, akatuma watu akawaua
watoto wote wanaume waliokuwako huko Bethlehemu na viungani mwake mwote, tangu
wenye miaka miwili na waliopungua, kwa muda ule aliouhakikisha kwa wale
mamajusi. Ndipo lilipotimia neno lililonenwa na nabii Yeremia, akisema, Sauti
ilisikiwa Rama, Kilio, na maombolezo mengi, Raheli akiwalilia watoto wake,
Asikubali kufarijiwa, kwa kuwa hawako.”
Mipango ya Herode na mikakati yake
na kughadhibika kwake kunaonyesha Dhahiri nia ya moyo wake ilikuwa ni
kuuufutilia mbali kabisa mpango wa Mungu, ni ujinga ulio wazi kuwa Herode
aliweza hata kuita wakuu wa makuhani na kuuliza kuwa masihi anazaliwa wapi na
akaelezwa kwa mujibu wa maandiko, lakini alikuwa amefanya upumbavu mkubwa sana
kwani nadhani alipaswa pia kuwauliza makuhani hao hao kuwa kuna madhara gani
anaweza kuyapata mtu anayejaribu kuzuia mapenzi ya Mungu? Na neno la Mungu lingemjibu hivi:-
Isaya 14:26-27 “Hilo ndilo kusudi
lililokusudiwa duniani mwote, na huo ndio mkono ulionyoshwa juu ya mataifa
yote. Maana Bwana wa majeshi amekusudia, naye ni nani atakayelibatili? Na mkono
wake ulionyoshwa, ni nani atakayeugeuza nyuma?”
Ayubu 9:4 “Yeye ni mwenye hekima moyoni, na
mwenye uwezo katika nguvu; Ni nani aliyejifanya kuwa mgumu juu yake, naye
akafanikiwa?”
Wakati wote, mahali popote na saa
yoyote kila mtu wa Mungu ni lazima ahahakikishe kuwa linapokuja swala ambalo ni
mapenzi ya Mungu, sisi kamwe tusiwe sababu ya kuharibu au kuzuia mpango huo
kwani kwa kufanya hivyo tunaweza kujikuta tunapingana na mapenzi ya Mungu jambo
ambalo ni hatari na linaweza kuleta madhara makubwa sana, tuache kiburi na
kujifikiri ya kuwa sisi ni maalumu sana, umaalumu wetu unaweza kuwa na maana
kama tuko kwaajili ya kutimiza mpango wake, lakini umaalumu wetu unaweza
kupotea ikiwa tu tunasimama kama kizuizi cha ule mpango halisi wa Mungu neno
linaonyeshqa huwezi kuwa mgumu kwa mapenzi ya Mungu kisha ukatoboa!
Matendo 5:38-39 “Basi sasa nawaambia,
Jiepusheni na watu hawa, waacheni; kwa kuwa shauri hili au kazi hii ikiwa
imetoka kwa binadamu, itavunjwa, lakini ikiwa imetoka kwa Mungu hamwezi
kuivunja; msije mkaonekana kuwa mnapigana na Mungu.”
Maandiko yanaonya vikali swala
zima la kujaribu kushindana na mapenzi ya Mungu, onyo linatolewa kuwa kama kazi
imetokana na binadamu inaweza kuvunjwa lakkini ikiwa imetokana na Mungu huwezi
kuvunja na kinyume chake mtu utakuwa
unajiingiza kwenye mfumo wa Mungu, nakumbushia kuwa Mungu habadiliki, Mungu
yule yule wa agano la kale ndiye huyu huyu wa Agano jipya, Rehema zake zinadumu
hata kizazi na kizazi kwa wamchao, lakini jicho lake li juu ya watenda mabaya
aliondoe kabisa kumbukumbu lao duniani.
Zaburi 34:15-16 “Macho ya Bwana huwaelekea
wenye haki, Na masikio yake hukielekea kilio chao. Uso wa Bwana ni juu ya
watenda mabaya, Aliondoe kumbukumbu lao duniani.”
Kwa maana wamekufa waliokuwa wakiitafuta roho ya Mtoto
Herode alikuwa moja ya wafalme
ambaye alishindana na kusudi la Mungu kuhusu Maisha ya Yesu, alikuwa anataka
kumwangamiza, alisahahu kujifunza kutoka kwa Farao ambaye mara kadhaa alikuwa
akikataa mpango wa Mungu wa kuwaachilia wana wa Israel waende katika nchi
iliyokusudiwa na Mungu na matokeo yake Taifa la Misri lilipatwa na mapigo
mazito yaliyosababisha hasara kubwa kwa Farao na raia wake na mwishoe msiba wa
wazaliwa wote wa kwanza wa binadamu na
wanyama uliwapata Misri nzima na kama haitoshi Farao na majeshi yake wote
walifutwa na Mungu katika bahari ya shamu, na hakukuweko mtu aliyesalia hata
kupeleka habari ya kile kilichowakuta!
Yeye ni mwenye akili moyoni, na
mwenye nguvu nyingi, ni nani aliyemwasi naye akasalimika? Herode aliyaasi
mapenzi ya Mungu na hivyo uwezo wake wa kuwa salama uliondolewa, kumbukumbu
lake duniani lilifutwa, huwezi kuufunga mpango wa Mungu kwa vizuizi vya
kibinadamu, Herode aliyatafuta sana maisha ya Yesu Kristo Mwana wa Mungu ili
kuyaangamiza na kwa dhamiri mbaya kabisa aliangamiza watoto wengi kule
Bethelehemu ili yamkini ikiwezekana miongoni mwao awe ni Bwana wetu Yesu
Kristo, Nini kilimtokea Herode maandiko yanaeleza tu kuwa alikufa ona:-
Mathayo 2:19-21 “Hata alipofariki Herode,
tazama, malaika wa Bwana alimtokea Yusufu katika ndoto huko Misri, akasema,
Ondoka, umchukue mtoto na mamaye, ushike njia kwenda nchi ya Israeli; kwa maana
wamekufa walioitafuta roho ya mtoto. Akaondoka akamchukua mtoto na mamaye,
akafika nchi ya Israeli.”
Hata hivyo Maandiko hayajaelezea
kwa kina yaliyomkuta Herode, lakini kwa taarifa za Mwandishi maarufu wa
kihistoria wa karne ya kwanza Myahudi Flavius Josephus anaelezea kuwa mara baada ya kuagiza askari
kuwaua watoto wadogo wasio na hatia kwa kusudi la kummaliza na Yesu, kule
Bethelehemu Mfalme huyo aliandamwa na maumivu
makali sana yasiyokoma, kujinyonga kwa utumbo mwembamba na kupata maumivu
makali sana, kubanwa na pumzi mfano wa mtu mwenye pumu, maumivu makali katika
kila sehemu ya mwili wake, mashambulizi makali ya figo, kumomonyoka kwa seli za
mwili wake (gangrene) na maambukizi
mabaya katika via vyake vya uzazi, kwa maelezo ya Mwanahitoria huyu nguli wa
kiyahudi anaeleza kuwa pia siku zake za mwisho akiwa na mashaka makubwa sana
aliuwa baadhi ya watoto wake wa kiume kwa hofu kuwa wangeweza kumpindua,
na mwisho aliagiza kuwa wakamatwe
viongozi muhimu wa kiyahudi na serikali yake na kuamuru kuwa wauawe siku
atakayokufa akiwa na mashaka kuwa hakuna mtu atakayeomboleza msiba wake kwa
vile alivyokuwa katili, kwa nini haya yalimkuta Herode? Kutokana na kupingana
na mapenzi ya Mungu na Mungu alimfutilia mbali ili mpango wa ukombozi kupitia
Yesu Kristo uweze kukaa katika njia yake na mapenzi ya Mungu yaweze kusimama!
Hitimisho:
-
Hakuna mwanadamu anaweza kuzuia mpango wa Mungu
hata siku moja iwe ndani ya mtu au katika agenda za Mungu nay ale ambayo watumishi wake manabii wamesema
-
Mungu ataendelea kuweka ulinzi dhidi ya wale
anaowatumia kwa mapenzi yake, na kujaribu kuwaharibu au kuharibu kitu cha Mungu
kilichomo ndani yao ni kujiweka katika wakati mbaya wa kuharibiwa wewe na Mungu
mwenyewe, Mungu huangalia maslahi yake mapana zaidi kuliko tamaa zako finyu, na
kutaka kwako kujijengea umaarufu acha kabisa kushindana na makusudi ya Mungu na
mpango wake.
-
Mungu akikugundua kuwa wewe ni kikwazo kwaajili
ya kazi yake atakuondoa kwa wakati wake ili mpango wake uweze kutimia, Maneno
haya wamekufa waliokuwa wakiitafuta roho ya mtoto yanadhihirisha wazi kuwa Mungu alisimamamia
kifo cha Herode ili mpango wake na agenda yake ndani ya Yesu Kristo iweze
kuendelea, Siku zote Mungu ataondoa kila kikwazo kinachosimama mbele ya watoto
wake ili makusudi yake yaweze kutimia,
do not mess-up with the G.O.D of Israel, usimkosee Mungu wa Wayahudi hata siku
moja
-
Kutoka
14:13-14 “Musa akawaambia watu, Msiogope, simameni
tu, mkauone wokovu wa BWANA atakaowafanyia leo; kwa maana hao Wamisri mliowaona
leo hamtawaona tena milele. BWANA atawapigania ninyi, nanyi mtanyamaza kimya.”
-
Tunajifunza kuwa Mungu huwapinga wenye kiburi,
lakini huwapa neema wanyenyekevu
Yakobo 4:6 Lakini
hutujalia sisi neema iliyozidi; kwa hiyo husema, Mungu huwapinga wajikuzao,
bali huwapa neema wanyenyekevu.”
Mtu yeyote anayezuia mapenzi ya
Mungu na kazi ya Mungu na makusudi ya Mungu hatadumu Mungu ana mwisho wa kila
Herode anayeitafuta roho ya mtoto aiangamize, ikiwa uko katika mpango wa Mungu
usiogope, kwani wanaoyatafuta maisha yako ili kuyaharibu wanaharibu ya kwao na
kwa ghafla kama ilivyokuwa kwa Herode kiburi chao kitafikia mwisho.
Na. Rev. Innocent Samuel Kamote
Mkuu wa wajenzi mwenye Hekima
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni