Jumatano, 29 Januari 2025

Kama umande wa Hermoni!


Zaburi 133:1-3 “Tazama, jinsi ilivyo vema, na kupendeza, Ndugu wakae pamoja, kwa umoja. Ni kama mafuta mazuri kichwani, Yashukayo ndevuni, ndevu za Haruni, Yashukayo mpaka upindo wa mavazi yake. Kama umande wa Hermoni ushukao milimani pa Sayuni. Maana ndiko Bwana alikoamuru baraka, Naam, uzima hata milele.”



Utangulizi:


Moja ya siri kubwa sana ya mafanikio ya kiroho na Baraka nyingi sana katika jamii yoyote ile, iwe Taifa, Kanisa, Familia, Ndoa, taasisi, na kadhalika yote yenye kujumuisha na kuwakutanisha watu Pamoja, umoja ni mojawapo ya nyenzo muhimu sana ya kusababisha Baraka nyingi. 


Mtumishi wa Mungu Daudi alilijua hili na akalizungumzia katika Zaburi ya 133, na kutuonyesha kuwa umoja unaleta upako, umoja unaleta Baraka, umoja unaleta uzima, tena hata uzima wa milele, Kimsingi Roho Mtakatifu hawezi kutenda kazi mahali ambapo kuna utengano, ubaguzi, upendeleo, ubinafsi, mafarakano na kukosekana kwa umoja, kwa kulijua hili Hata Bwana wetu Yesu Kristo aliwaombea wanafunzi wake yaani ikiwa ni pamoja na wewe na mimi kuwa tuwe na umoja 


Yohana 17:11-12. “Wala mimi simo tena ulimwenguni, lakini hawa wamo ulimwenguni, nami naja kwako. Baba mtakatifu, kwa jina lako ulilonipa uwalinde hawa, ili wawe na umoja kama sisi tulivyo.Nilipokuwapo pamoja nao, mimi naliwalinda kwa jina lako ulilonipa, nikawatunza; wala hapana mmojawapo wao aliyepotea, ila yule mwana wa upotevu, ili andiko litimie.” 


Mpango wangu leo sio kuzungumzia kuhusu umoja, lakini Bwana amenituma kuzunguzia faida za umoja, au matokeo yanayoletwa na Umoja, Daudi anaona wema unaotokana na watu kukaa kwa umoja na anaelezea matokeo yake, au faida zake na anatoa mifano miwili, mmoja ni Mafuta mazuri kutoka kichwani, na pili umande wa Hermoni unaoshukia Sayuni, kimsingi Daudi anazungumzia Upako na Umande ambao ni matokeo ya Baraka za Roho Mtakatifu. Na kubwa zaidi nitazungumzia hili la “Kama umande wa Hermoni” tutajifunza somo hili kama umande wa Hermoni kwa kuzingatia vipengele vitatu vifuatavyo:-


Umuhimu wa umande.

Kama umande wa Hermoni.

Jinsi ya kufunikwa na umande.



Umuhimu wa umande.

Ni muhimu kufahamu kuwa umande katika lugha ya kiebrania unaitwa “ţal” kwa kiingereza unaitwa “dew” umande una umuhimu mkubwa sana katika nchi sawasawa tu na mvua ilivyo na umuhimu, wale wanaoishi katika inchi zenye mfumo wa kuweko kwa umande watakuwa wanafahamu jinsi umande ulivyo wa muhimu, inchi ikikosa mvua hakuna tofauti na inchi ikikosa umande, Wayahudi walikuwa na uelewa mkubwa sana kuhusu umuhimu wa umande, ukweli ni kuwa kunyimwa mvua pamoja na umande ilikuwa ni hukumu kubwa sana ni janga


1Wafalme 17:1 “Basi Eliya Mtishbi, wa wageni wa Gileadi, akamwambia Ahabu, Kama Bwana, Mungu wa Israeli, aishivyo, ambaye ninasimama mbele zake, hakutakuwa na UMANDE wala mvua miaka hii, ila kwa neno langu.”


Umande katika historia ya Israel uliwakilisha uwepo wa Mungu, umande ulikuwa na umuhimu mkubwa sana kama ilivyo mvua, ulikuwa na manufaa makubwa sana kwao, umande uliifanya nchi iwe na utulivu na kupoa kutoka katika joto la jangwa, ulileta utulivu kwa wanadamu, umande huifanya nchi iwe na hali joto lenye kupendeza sana, umande unaifanya ardhi iwe tayari kupokea mbegu njema na kustawi, umande kuondoka ilikuwa sawa tu na uwepo wa Mungu kuondoka, Mungu alikuwa amewathibitishia Israel kuwa atakuwa pamoja nao kama umande, umande unapokuwepo kila kitu kinastawi na umande unapokauka hali huwa mbaya 


Hosea 14:4-6 “Mimi nitawaponya kurudi nyuma kwao; nitawapenda kwa ukunjufu wa moyo; kwa maana hasira yangu imemwacha. NITAKUWA KAMA UMANDE kwa Israeli; naye atachanua maua kama nyinyoro, na kuieneza mizizi yake kama Lebanoni. Matawi yake yatatandaa, na uzuri wake utakuwa kama uzuri wa mzeituni, na harufu yake kama Lebanoni.”


Israel walipokuwa jangwani wote tunakumbuka jinsi Mungu alivyowalisha kwa mana, lakini wote tunakumbuka kuwa mana ilishuka pamoja na umande, na umande ulikuwa ukiondoka basi muda wa kuokota mana ungeondoka na umande, na jua lingechukua nafasi yake na hivyo kusingeliweko na mana tena, kwa hiyo ujio wa Mana wakati wote uliambatana na umande 


Kutoka 16:13-15 “Ikawa wakati wa jioni, kware wakakaribia, wakakifunikiza kituo; na wakati wa asubuhi umande ulikuwa juu ya nchi pande zote za kituo. NA ULIPOINUKA ULE UMANDE uliokuwa juu ya nchi, kumbe! Juu ya uso wa bara kitu kidogo kilichoviringana, kidogo kama sakitu juu ya nchi. Wana wa Israeli walipokiona, wakaambiana, Nini hiki? Maana hawakujua ni kitu gani. Musa akawaambia, Ndio mkate ambao BWANA amewapa ninyi, mle.”


Hesabu 11:7-9 “Na hiyo mana ilikuwa mfano wa chembe za mtama na kuonekana kwake kulikuwa kama kuonekana kwake bedola. Watu wakazunguka-zunguka na kuikusanya, kisha wakaisaga kwa mawe ya kusagia, au kuitwanga katika vinu, kisha wakaitokosa nyunguni, na kuandaa mikate; na tamu yake ilikuwa kama tamu ya mafuta mapya. UMANDE ULIPOYAANGUKIA MARAGO WAKATI WA USIKU, HIYO MANA ILIANGUKA PAMOJA NAO.”


Wana wa Israel walifahamu umuhimu wa umande, Umande ulikuja na mana, na ni umande ulioifanya mana isichafuke japo iliangukia juu ya nchi, lakini nchi haikuweza kuichafua mana kwa sababu ilikuja na UMANDE, Endapo wote tunakubaliana kuwa Mana ni mkate kutoka mbinguni na unamwakilisha Yesu, basi vile vile utakubaliana nami kuwa Umande unawakilisha uwepo wa Roho Mtakatifu, Hakuna Baraka kubwa kwa kanisa kama kuwa na Roho Mtakatifu, yeye analeta wakati wa kuburudishwa na kuondoa kila aina ya hali ya ukavu wa kiroho, katika kanisa na kutuletea uamsho na wakati mzuri wa kufanya naye kazi, bila kupigwa na jua, sasa kwa mujibu wa Daudi kama watu wanataka kuburudishwa na kufurahia Baraka za Mungu siri imejificha katika wema wa kukaa kwa umoja, na hii ndio kanuni muhimu ya kanisa kuwa na uamsho, na zaidi ya yote kama ulijifunza kuwa katika alama za Roho Mtakatifu ni pamoja na njiwa, moto, maji, mafuta, wingu, kisima, mito ya maji, na upepo, leo nakuongezea na UMANDE. 


Kama umande wa Hermoni.


Zaburi 133:1-3 “Tazama, jinsi ilivyo vema, na kupendeza, Ndugu wakae pamoja, kwa umoja. Ni kama mafuta mazuri kichwani, Yashukayo ndevuni, ndevu za Haruni, Yashukayo mpaka upindo wa mavazi yake. KAMA UMANDE WA HERMONI ushukao milimani pa Sayuni. Maana ndiko Bwana alikoamuru baraka, Naam, uzima hata milele.”


Kwa nini kama umande wa Hermoni? Mlima Mlima Hermoni ni Moja ya safu za milima yenye urefu wa maili 30, na upana wa maili 15 urefu wake kwenda juu ni futi zaidi ya 9000 kutoka usawa wa bahari, safu hii ya milima imefunikwa na theluji kama unavyoweza kuona pichani, Milima hii iko kaskazini mashariki mwa Israel katika mpaka wa Syria na Lebanon Mlima huu una utajiri mkubwa sana wa kusababisha mvua, lakini pia una chemichemi za maji na zaidi ya yote ni chanzo kikuu cha mto Yordani, lakini mlima huu pia husababisha umande katika Sayuni au Israel kwa hiyo Daudi anauona mlima huu kama chanzo cha Baraka kubwa sana kwa Israel, Daudi anaona kuwa watu wakikaa kwa umoja Mungu huachilia Baraka zake na ustawi sawa na mlima huu unavyotumiwa na Mungu kuwa chanzo kikubwa cha mafanikio ya kilimo kwa Israel, Ni katika mlima huu pia ndiko inakohisiwa kuwa Yesu alipanda na wanafunzi wake na kugeuka sura yake MLIMA MREFU FARAGHANI


Mathayo 17:1-8 “Na baada ya siku sita Yesu akawatwaa Petro, na Yakobo, na Yohana nduguye, akawaleta juu ya mlima mrefu faraghani; akageuka sura yake mbele yao; uso wake ukang'aa kama jua, mavazi yake yakawa meupe kama nuru. Na tazama, wakatokewa na Musa na Eliya, wakizungumza naye. Petro akajibu akamwambia Yesu, Bwana, ni vizuri sisi kuwapo hapa; ukitaka, nitafanya hapa vibanda vitatu, kimoja chako wewe, na kimoja cha Musa, na kimoja cha Eliya. Alipokuwa katika kusema, tazama, wingu jeupe likawatia uvuli; na tazama, sauti ikatoka katika lile wingu, ikasema, Huyu ni Mwanangu, mpendwa wangu, ninayependezwa naye; msikieni yeye. Na wale wanafunzi waliposikia, walianguka kifulifuli, wakaogopa sana.”


2Petro 1:16-18 “Maana hatukufuata hadithi zilizotungwa kwa werevu, tulipowajulisha ninyi nguvu zake Bwana wetu Yesu Kristo na kuja kwake; bali tulikuwa tumeuona wenyewe ukuu wake. Maana alipata kwa Mungu Baba heshima na utukufu, hapo alipoletewa sauti iliyotoka katika utukufu mkuu, Huyu ni Mwanangu, mpendwa wangu, ninayependezwa naye. Na sauti hiyo sisi tuliisikia ikitoka mbinguni tulipokuwa pamoja naye katika mlima ule mtakatifu.” 


Kwa ujumla Ustawi mzima wa Israel unategemea sana mlima wa Hermoni, na ndio maana Daudi anasema huko ndiko Mungu alikoziamuru Baraka, na kwanini anasema hivyo kwa sababu umande pia katika Israel unaungamanishwa na baraka, hakuna mahali popote pale katika Biblia mtu alibarikiwa kisha neno UMANDE lisitajwe, wakati wote wazee katika Biblia walipotamka baraka walimtamkia mtu kuwa na UMANDE kama neema na baraka kubwa sana kutoka mbinguni kwa hiyo kutamkiwa ya UMANDE katika maisha ya mwanadamu ni ishara ya Baraka ona:-


Mwanzo 27:27-29 “Akakaribia akambusu. Naye akasikia harufu ya mavazi yake, akambariki akasema, Tazama, harufu ya mwanangu Ni kama harufu ya shamba alilolibariki BWANA. MUNGU NA AKUPE YA UMANDE WA MBINGU, Na ya manono ya nchi, Na wingi wa nafaka na mvinyo. Mataifa na wakutumikie Na makabila wakusujudie, Uwe bwana wa ndugu zako, Na wana wa mama yako na wakusujudie. Atakayekulaani alaaniwe, Na atakayekubariki abarikiwe.” 


Mwanzo 27:39 “Esau akamwambia babaye, Una mbaraka mmoja tu, babangu? Unibariki mimi, mimi nami, Ee babangu. Esau akapaza sauti yake, akalia. Isaka, baba yake, akajibu, akamwambia, Angalia, penye manono ya nchi patakuwa makao yako, NA PENYE UMANDE WA MBINGU UNAOTOKA JUU.”


Kumbukumbu 33:13-15 “Na Yusufu akamnena, Nchi yake na ibarikiwe na Bwana; Kwa vitu vya thamani vya mbinguni, KWA HUO UMANDE, Na kwa kilindi kilalacho chini, Na kwa vitu vilivyo bora vya matunda ya jua, Na kwa vitu vilivyo bora vya maongeo ya miezi, Na kwa vitu viteule vya milima ya kale, Na kwa vitu vilivyo bora vya vilima vya milele,”


Mika 5:7-9 “Na hayo mabaki ya Yakobo yatakuwa kati ya kabila nyingi MFANO WA UMANDE UTOKAO KWA BWANA, mfano wa manyunyu katika manyasi; yasiyomngojea mtu, wala kuwakawilia wanadamu.Na hayo mabaki ya Yakobo yatakuwa kati ya mataifa, kati ya kabila nyingi, mfano wa simba kati ya wanyama wa msituni, kama mwana-simba kati ya makundi ya kondoo, ambaye, akiwa anapita katikati, hukanyaga-kanyaga na kurarua-rarua, wala hakuna wa kuokoa.Mkono wako na uinuliwe juu ya adui zako, na adui zako wote wakauliwe mbali.” 


Ayubu 29:19-20 “Shina langu limeenea hata kufika majini, NA UMANDE hukaa usiku kucha katika matawi yangu; Utukufu wangu utakuwa mpya kwangu, Na uta wangu hurejezwa upya mkononi mwangu.”


Unaona? Kwa hiyo Umande ni alama ya Baraka, umande ni alama ya ustawi, umande ni alama ya kuburudishwa, umande ni alama ya Roho Mtakatifu na matunda yake, Baraka hizi tunaweza kuziona kwa sharti la kukaa pamoja na kwa umoja, hatuwezi kukaa pamoja na kwa umoja kama hakuna msamaha, kama hakuna umoja, kama hakuna upendo, kama hakuna amani, kama hakuna furaha, kama hakuna kiasi, kama hakuna adabu, kama hakuna uvumilivu, kama hakuna kutokuhesabu mabaya, kama hakuna kuchukuliana, kama hakuna kujaliana, kama hakuna kula pamoja, kama hakuna ushirikiano, kama kuna ubinafsi, kama kuna mimi kwanza, kama kuna kujiona bora, kama kuna kusengenyana, kama kuna kuchafuana, kama kuna kuchokana, kama hakuna fadhili, kama kuna husuda, kama kuna kujivuna, kama kuna kiburi, kama kuna uchungu, kama kuna udhalimu, kama hakuna ukweli, kama kuna fitina, kama kuna majungu, kama kuna wivu, kama kuna uadui, kama kuna uzushi, kama kuna husuda, kama kuna kurogana na kuharibiana, kama kuna mashindano, Mungu hataweza kuamuru Baraka zake kuja kwetu kama hatuna ukomavu wa kutosha na kufikia hatua ya kuchukuliana unataka Baraka za Mungu zije kwako kumbuka, unataka Mungu aziamuru Baraka kumbuka kumbuka, katika Taifa, katika Kanisa, katika ndoa, katika taasisi, katika mashirika, katika kampuni, katika biashara, kote tutaziona Baraka za Mungu ikiwa tu tutakaa kwa umoja, Mungu ataachilia upako wake kwa kila kiungo katika mwili wa Kristo na ataachilia Baraka zake kama umande wa Hermoni katika maisha yetu yote   


Jinsi ya kufunikwa na umande.


Mtafute Mungu kwanza – Kama hauna uhusiano mzuri na Mungu hakikisha kuwa unautafuta kwanza uso wake, unatafuta kuwa na uhusiano mzuri na Mungu, yeye ndiye chanzo cha Baraka zote yaani UMANDE endapo utautafuta uso wake hakuna kitu ambacho Mungu atakunyima kwa sababu Mungu amekusudia kumbariki kila mmoja 


Mathayo 6:31-33 “Msisumbuke, basi, mkisema, Tule nini? Au Tunywe nini? Au Tuvae nini? Kwa maana hayo yote Mataifa huyatafuta; kwa sababu Baba yenu wa mbinguni anajua ya kuwa mnahitaji hayo yote. Bali utafuteni kwanza ufalme wake, na haki yake; na hayo yote mtazidishiwa.”


Mwabudu yeye – Ulimwengu wa roho unaachilia vitu kwa ibada ukimuabudu shetani atakupa heshima, mali na utajiri wa dunia lakini nafsi yako itaangamia, lakini ukimtumikia Mungu na kumtii hiyo ndiyo ibada ataziachilia Baraka zake na zitakupata 


Mathayo 4:8-10 “Kisha Ibilisi akamchukua mpaka mlima mrefu mno, akamwonyesha milki zote za ulimwengu, na fahari yake, akamwambia, Haya yote nitakupa, ukianguka kunisujudia. Ndipo Yesu alipomwambia, Nenda zako, Shetani; kwa maana imeandikwa, Msujudie Bwana Mungu wako, umwabudu yeye peke yake.”


Kumbukumbu 28:1-8 “Itakuwa utakaposikia sauti ya Bwana, Mungu wako, kwa bidii, kutunza kuyafanya maagizo yake yote nikuagizayo leo, ndipo Bwana, Mungu wako, atakapokutukuza juu ya mataifa yote ya duniani; na baraka hizi zote zitakujilia na kukupata usikiapo sauti ya Bwana, Mungu wako. Utabarikiwa mjini, utabarikiwa na mashambani. Utabarikiwa uzao wa tumbo lako, na uzao wa nchi yako, na uzao wa wanyama wako wa mifugo, maongeo ya ng'ombe wako, na wadogo wa kondoo zako. Litabarikiwa kapu lako, na chombo chako cha kukandia unga. Utabarikiwa uingiapo, utabarikiwa na utokapo. Bwana atawafanya adui zako wainukao juu yako kupigwa mbele yako; watakutokea kwa njia moja, lakini watakimbia mbele yako kwa njia saba. Bwana ataiamuru baraka ije juu yako katika ghala zako, na mambo yote utakayotia mkono wako; naye atakubarikia katika nchi akupayo Bwana, Mungu wako.”  


Kuwa na Amani na watu wote – Uhusiano wetu hauwezi kuwa kamili kama tutakuwa na madai kuwa tunampenda Mungu huku hatuwajali wengine, huna Amani na watu wengine maana yake hakuna umoja, Mungu hawezi kuachilia Baraka zake kwa watu wenye mafarakano, ndio maana moja ya silaha kubwa anayoitumia shetani katika kanisa, taifa, familia, taasisi na kdhalika ni pamoja na kuondoa umoja. Kwa kuvuruga Amani.


Waebrania 12:14 “Tafuteni kwa bidii kuwa na amani na watu wote, na huo utakatifu, ambao hapana mtu atakayemwona Bwana asipokuwa nao;”


Acha kuwa mwilini - Acha ukristo wa mwilini, jikaze, onyesha ukomavu, jionyeshe kuwa mwanaume, onyesha kukua, uwe na uwezo wa kusamehe na kuachilia, wewe kila siku una yale yale tu, fungua moyo wako kubali kukua kiroho, usiweke mtu moyoni, usimchafue nduguyo, kuwa na amani na watu wote maana yake hata wale waliokukosea, wakati mwingine usisubiri waje kukuomba msamaha wewe achilia au nenda kaombe Amani usijifungie kwenye gereza la kukosa mafanikio utajichelewesha

 

1Wafalme 2:1-3 “Basi siku ya kufa kwake Daudi ikakaribia, akamwusia Sulemani mwanawe, akasema, Mimi naenda njia ya ulimwengu wote; basi uwe hodari, ujionyeshe kuwa mwanamume; uyashike mausia ya Bwana, Mungu wako, uende katika njia zake, uzishike sheria zake, na amri zake, na hukumu zake, na shuhuda zake, sawasawa na ilivyoandikwa katika torati ya Musa, upate kufanikiwa katika kila ufanyalo, na kila utazamako;”


1Wakorintho 3:1-3 “Lakini, ndugu zangu, mimi sikuweza kusema nanyi kama na watu wenye tabia ya rohoni, bali kama na watu wenye tabia ya mwilini, kama na watoto wachanga katika Kristo.Naliwanywesha maziwa sikuwalisha chakula; kwa kuwa mlikuwa hamjakiweza. Naam, hata sasa hamkiwezi,kwa maana hata sasa ninyi ni watu wa tabia ya mwilini. Maana, ikiwa kwenu kuna husuda na fitina, je! Si watu wa tabia ya mwilini ninyi; tena mnaenenda kwa jinsi ya kibinadamu?  

  

Acha uchoyo uwe mtoaji – Neno la Mungu limesema ni heri kutoa kuliko kupokea, wewe hutoi, umekuwa mchoyo kila kitu kizuri unajilimbikizia na kutaka kiwe chako, unataka Baraka za Mungu ili iweje? Ili uringishie watu? Ili uwakanyage watu kichwani? Ili uwe na mamalaka juu ya watu? Mungu amekusudia kutubariki ili tuwe baraka Kwa wengine.


Matendo 20:33-35 “Sikutamani fedha wala dhahabu, wala mavazi ya mtu. Ninyi wenyewe mnajua ya kuwa mikono yangu hii imetumika kwa mahitaji yangu na ya wale waliokuwa pamoja nami.Katika mambo yote nimewaonyesha ya kuwa kwa kushika kazi hivi imewapasa kuwasaidia wanyonge, na kuyakumbuka maneno ya Bwana Yesu, jinsi alivyosema mwenyewe, Ni heri kutoa kuliko kupokea.” 


Tumejifunza kuwa UMANDE unawakilisha Baraka za Mungu na baraka hizi za Mungu ni pamoja na uwepo wake na upako wa Roho Mtakatifu, lakini ili tuweze kufunikwa na baraka hizo ni lazima tuyatende mambo yale yote ambayo katika jamii yanatufanya tuwe na umoja na amani na kuacha yale yote yanayotufarakanisha tukiwa na umoja katika jambo lolote lile tutafanikiwa, kwa umri wangu huu nimeona taasisi zikifa, zikiharibika, na kudumaa kwa sababu tu watu walitanguliza maslahi yao mbele na wakaacha kuwajali wengine na wakavuruga umoja na kuondoa Amani na matokeo yake ikawa ni ukiwa, Mungu anapoona ya kuwa hatumjali yeye wala hatutendeani kwa hisani basi, atamtuma nabii wake ambaye atatangaza kuwa hapatakuwa na mvua wala umande………  


Na. Mchungaji Innocent Kamote


Mkuu wa wajenzi mwenye Hekima.

Jumatano, 22 Januari 2025

Mungu ajibuye kwa Moto!


1Wafalme 18:20-24 “Basi, Ahabu akapeleka watu kwa wana wa Israeli wote, akawakusanya manabii pamoja katika mlima wa Karmeli. Naye Eliya akawakaribia watu wote, akanena, Mtasita-sita katikati ya mawazo mawili hata lini? Bwana akiwa ndiye Mungu, mfuateni; bali ikiwa Baali ni Mungu, haya! Mfuateni yeye. Wale watu hawakumjibu neno. Ndipo Eliya akawaambia watu, Mimi nimesalia, mimi peke yangu, nabii wa Bwana; lakini manabii wa Baali ni watu mia nne na hamsini. Kwa hiyo na watutolee ng'ombe wawili; wao na wajichagulie ng'ombe mmoja, wamkate-kate na kumweka juu ya kuni, wasitie moto chini; nami nitamtengeza huyo ng'ombe wa pili, na kumweka juu ya kuni, wala sitatia moto chini. Nanyi ombeni kwa jina la mungu wenu, nami nitaomba kwa jina la Bwana; na Mungu yule ajibuye kwa moto, na awe ndiye Mungu. Watu wote wakajibu wakasema, Maneno haya ni mazuri.



Utangulizi:

Ni muhimu kufahamu kuwa mojawapo ya njia ya kupambana na manabii wa uongo, sio tu kuwajibu kwa mafundisho peke yake, lakini ni pamoja na ishara na miujiza inayoambatana na utendaji wa Roho Mtakatifu, katika maisha ya watumishi na Kanisa kwa ujumla. Wakati mwingine ili Mungu wa kweli apate kujulikana ni lazima ishara mashuhuri zifanyike, ili watu wapate kuamini kuwa Mungu ni mwenye nguvu, Ishara na miujiza ni ya Muhimu sana katika kuthibitisha uweza na nguvu za Mungu.

Kutoka 7:10-12 “Basi Musa na Haruni wakaingia kwa Farao, wakafanya vivyo kama BWANA alivyowaambia; Haruni akaibwaga fimbo yake chini mbele ya Farao, mbele ya watumishi wake, ikawa nyoka. Ndipo Farao naye akawaita wenye akili na wachawi; na hao waganga wa Misri wakafanya vivyo kwa uganga wao. Wakabwaga chini kila mtu fimbo yake, nazo zikawa nyoka; lakini fimbo ya Haruni ikazimeza fimbo zao.”

Mungu amewapa watumishi wake Ishara na miujiza kwa uweza wa Roho wake Mtakatifu kwaajili ya kusaidia watu lakini wakati mwingine kama ishara kwa wasioamini wapate kuamini na kuondoka katika hali ya mashaka na kusita sita, Wakati wa Nabii Eliya jamii kubwa ya wana wa Israel walikuwa wamepoteza njia sahihi ya kumuabudu Mungu na wengi walikuwa wamegeukia miungu mingine wakiabudu miungu ya kikanaani akiwemo Baali, kwa hiyo ulifikia wakati wakaanza kuchanganya ibada za Mungu wa kweli na ibada za Baali, kimsingi walikuwa ni watu wenye kusitasita katika mawazo mawili. Eliya akilielewa hili huku moyoni mwake akiwa na agizo la kuirejesha mioyo ya wana wa Israel katika ibada ya Mungu wa kweli yeye alitoa wazo, ambalo liliungwa mkono na manabii wa Baali na watu wote kwamba ufikie wakati sasa Mungu yule atakayejibu kwa Moto huyo awe ndiye Mungu wa kufuatwa na kuabudiwa. Tutajifunza somo hili kwa kuzingatia vipengele vitatu vifuatavyo:-


Mtasita-sita katikati ya mawazo mawili hata lini?

Mungu yule ajibuye kwa moto

Mwisho wa Manabii wa uongo


Mtasita-sita katikati ya mawazo mawili hata lini?

Moja ya mambo ambayo yanamuudhi sana Mungu ni pamoja na kuwa na mtu au watu wenye kusitasita, Mungu anavutiwa sana na mtu au watu wanaofanya maamuzi, Mara kwa mara Mungu kupitia watumishi wake kadhaa amewahi kuwapa changamoto wanadamu kufanya maamuzi ya kuchagua, kila siku katika maisha yetu tunaweza au tumepewa kuchagua, unaweza kuchagua uzima au mauti, unaweza kuchagua laana au baraka, unaweza kuchagua Mungu au miungu, unaweza kuchagua kuwa moto au baridi, Kuchagua upande mmoja ndio njia sahihi, na kusisita katika mawazo mawili sio sahihi na ni jambo ambalo linamchukiza sana Mungu na kumnyima furaha.

Kumbukumbu 30:15-16. “Angalia, nimekuwekea leo mbele yako uzima na mema, na mauti na mabaya; kwa hivi nikuagizavyo leo kumpenda Bwana, Mungu wako, kuenenda katika njia zake, na kushika maagizo yake, na amri zake, na hukumu zake, upate kuwa hai na kuongezeka; Bwana, Mungu wako, apate kukubarikia katika nchi uingiayo kuimiliki.”

Kumbukumbu 11:26-28 “Angalieni, nawawekea mbele yenu hivi leo baraka na laana;baraka ni hapo mtakapoyasikiza maagizo ya Bwana, Mungu wenu, niwaagizayo leo; na laana ni hapo msiposikiza maagizo ya Bwana, Mungu wenu, mkikengeuka katika njia niwaagizayo leo, kwa kuandama miungu mingine msiyoijua.”

Yoshua 24:14-15 “Basi sasa mcheni Bwana, mkamtumikie kwa unyofu wa moyo na kwa kweli; na kuiweka mbali miungu ambayo baba zenu waliitumikia ng'ambo ya Mto, na huko Misri; mkamtumikie yeye Bwana.Nanyi kama mkiona ni vibaya kumtumikia Bwana, chagueni hivi leo mtakayemtumikia; kwamba ni miungu ile ambayo baba zenu waliitumikia ng'ambo ya Mto, au kwamba ni miungu ya wale Waamori ambao mnakaa katika nchi yao; lakini mimi na nyumba yangu tutamtumikia Bwana.” 

Ufunuo 3:15-16 “Nayajua matendo yako, ya kuwa hu baridi wala hu moto; ingekuwa heri kama ungekuwa baridi au moto. Basi, kwa sababu una uvuguvugu, wala hu baridi wala moto, nitakutapika utoke katika kinywa changu.” 

Waebrania 10:38 “Lakini mwenye haki wangu ataishi kwa imani; Naye akisita-sita, roho yangu haina furaha naye.

Maisha yetu ni uchaguzi, Maandiko yanashauri tumchague Mungu lakini tusibaki katikati, kumchagua Mungu ni Baraka kubwa sana na kuacha kumchagua Mungu ni laana, Mungu hapandezwi wala havutiwi na watu wanaositasita, wala havutiwi na watu vuguvugu, Mungu anataka tuwe moto na tumchague yeye kumchagua yeye ni kuchagua mafanikio, tatizo lililoko leo halina tofauti na tatizo lililokuweko wakati wa Eliya, jamii ya watu katika Israel walikuwa wanasitasita, walikuwa vugu vugu, walikuwa wakichanganya ibada ya Mungu mwenyezi na miungu ya Kanaani ya Baali, Eliya alitokea kama nabii aliyesalia peke yake na wengi walikuwa wakimuabudu Baali, akaamua kuweka changamoto ya kitaifa, kuanzia na mfalme kwamba watu wote wafanye uamuzi na Mungu halisi wa kweli ajulikane kuwa Mungu ili afuatwe, Eliya alikuja sio tu na swali lakini alikuja na suluhu ya changamoto iliyokuwa inawakabili watu, Eliya alisema

 “manabii wa Baali ni watu mia nne na hamsini. Kwa hiyo na watutolee ng'ombe wawili; wao na wajichagulie ng'ombe mmoja, wamkate-kate na kumweka juu ya kuni, wasitie moto chini; nami nitamtengeza huyo ng'ombe wa pili, na kumweka juu ya kuni, wala sitatia moto chini” 

katika mjadala huu na hoja hii Eliya aliwapa changamoto kuwa moto utoke kwa Mungu, kama manabii wa baali wana mungu kwa kweli basi sadaka yao itatiwa moto na Baali na kama Mungu anayewakilishwa na Eliya ni wa kweli basi sadaka yake itatiwa moto na Mungu mwenyezi na wazo hilo lilikuwa jema na lilikubalika ili kuumaliza utata.

1Wafalme 18:20-24 “Basi, Ahabu akapeleka watu kwa wana wa Israeli wote, akawakusanya manabii pamoja katika mlima wa Karmeli. Naye Eliya akawakaribia watu wote, akanena, Mtasita-sita katikati ya mawazo mawili hata lini? Bwana akiwa ndiye Mungu, mfuateni; bali ikiwa Baali ni Mungu, haya! Mfuateni yeye. Wale watu hawakumjibu neno. Ndipo Eliya akawaambia watu, Mimi nimesalia, mimi peke yangu, nabii wa Bwana; lakini manabii wa Baali ni watu mia nne na hamsini. Kwa hiyo na watutolee ng'ombe wawili; wao na wajichagulie ng'ombe mmoja, wamkate-kate na kumweka juu ya kuni, wasitie moto chini; nami nitamtengeza huyo ng'ombe wa pili, na kumweka juu ya kuni, wala sitatia moto chini. Nanyi ombeni kwa jina la mungu wenu, nami nitaomba kwa jina la Bwana; na Mungu yule ajibuye kwa moto, na awe ndiye Mungu. Watu wote wakajibu wakasema, Maneno haya ni mazuri.

Mungu yule ajibuye kwa moto

Eliya alikuwa anajua kwamba ili kumaliza utata kuna umuhimu wa kufanya ishara mashuhuri, Na muujiza huu ambao ulifanyika kando ya mlima Karmel ulikuwa ni wa muhimu sana na umeweka alama ya kipekee katika historia ya Israel, kutokana na umashuhuri wake, Karmel kwa kiebrania (ho Kármelos maana yake ni bustani ya matunda hata hivyo kutokana na ishara kubwa na muujiza uliofanyioka hapo watu wengi sana hupaita mahali hapo Mlima wa Moto) Ishara mashuhuri inapofanyika huwanyima maadui uwezo wa kujibu hoja na kukosa mashiko ya kile wanachokisimamia, Ishara mashuhuri ni lile tukio ambalo Mungu hulifanya na macho ya watu wote wakishuhudia kwa macho ya nyama yaani sio kwa kutilia shaka, Mfano Yesu alipomfufua Lazaro, ambaye alikuwa amezikwa siku nne na taarifa zake zilijulikana sana, au mfano wa Mlemavu ambaye Petro na Yohana walimsaidia kwenye mlango mzuri ambaye alikuwa anajulikana na jamii nzima kuwa anaomba omba, watu wale ambao dunia inawajua, mji unajua, nchi inajua na taifa linajua na maadui wa Mungu hawawezi kuikana ishara hiyo hiyo huitwa ishara mashuhuri, hiki ndicho ambacho Eliya alikuwa amekikusudia kifanyike ili dunia yote na taifa zima liweze kukubali na kuamini ya kwamba Adonai ndiye Mungu wa kweli ilikuwa ni lazia lifanyike tukio ambalo sio la kawaida.

Matendo 4:15-16 “Wakawaamuru kutoka katika baraza, wakafanya shauri wao kwa wao, wakisema, Tuwafanyie nini watu hawa? Maana ni dhahiri kwa watu wote wakaao Yerusalemu ya kwamba ishara mashuhuri imefanywa nao, wala hatuwezi kuikana.” 

Jamii nzima ilikubaliana na tukio hilo na manabii wa Baali walikuwa wakwanza kuomba nadhani ilikuwa asubuhi kuanzia mida ya saa tatu mpaka jioni kwenye saa tisa, na kisha saa tisa Eliya alichukua nafasi naye na kuomba na hivi ndivyo mambo yalivyokuwa:-

1Wafalme 18:25-39 “Eliya akawaambia manabii wa Baali, Jichagulieni ng'ombe mmoja, mkamtengeze kwanza; maana ninyi ndio wengi; mkaliitie jina la mungu wenu, wala msitie moto chini. Wakamtwaa yule ng'ombe waliyepewa, wakamtengeza, wakaliitia jina la Baali tangu asubuhi hata adhuhuri, wakisema, Ee Baali, utusikie. Lakini hapakuwa na sauti, wala aliyejibu. Nao wakaruka-ruka juu ya madhabahu waliyoifanya. Ikawa, wakati wa adhuhuri, Eliya akawafanyia dhihaka, akasema, Mwiteni kwa sauti kuu; maana ni mungu huyo; labda anazungumza, au ana shughuli, au anasafiri, au labda amelala, sharti aamshwe. Wakapiga kelele, wakajikata-kata kwa visu na vyembe kama ilivyo desturi yao, hata damu ikawachuruzika. Ikawa, wakati wa adhuhuri ulipopita, walitabiri hata wakati wa kutoa dhabihu ya jioni; lakini hapakuwa na sauti, wala aliyejibu, wala aliyeangalia. Kisha Eliya akawaambia watu wote, Nikaribieni mimi. Watu wote wakamkaribia. Akaitengeneza madhabahu ya Bwana iliyovunjika. Eliya akatwaa mawe kumi na mawili, kwa hesabu ya kabila za wana wa Yakobo, aliyejiliwa na neno la Bwana na kuambiwa, Jina lako litakuwa Israeli. Naye akaijenga madhabahu kwa mawe hayo katika jina la Bwana; akafanya mfereji, kama wa vipimo viwili vya mbegu, ukiizunguka madhabahu. Kisha akazipanga zile kuni, akamkata yule ng'ombe vipande vipande, akaviweka juu ya kuni. Akasema, Jazeni mapipa manne maji, mkayamwage juu ya sadaka ya kuteketezwa, na juu ya kuni. Akasema, Fanyeni mara ya pili. Wakafanya mara ya pili. Akasema, Fanyeni mara ya tatu. Wakafanya mara ya tatu. Yale maji yakaizunguka madhabahu; akaujaza mfereji maji. Ikawa, wakati wa kutoa dhabihu ya jioni, Eliya nabii akakaribia, akasema, Ee Bwana, Mungu wa Ibrahimu, na wa Isaka, na wa Israeli, na ijulikane leo ya kuwa wewe ndiwe Mungu katika Israeli, na ya kuwa mimi ni mtumishi wako, na ya kuwa nimefanya mambo haya yote kwa neno lako. Unisikie, Ee Bwana, unisikie, ili watu hawa wajue ya kuwa wewe, Bwana, ndiwe Mungu, na ya kuwa wewe umewageuza moyo wakurudie. Ndipo moto wa Bwana ukashuka, ukaiteketeza sadaka ya kuteketezwa, na kuni, na mawe, na mavumbi, ukayaramba yale maji yaliyokuwamo katika mfereji. Na watu wote walipoona, wakaanguka kifudifudi; wakasema, Bwana ndiye Mungu, Bwana ndiye Mungu.”

Unaona? Eliya hakufanya mambo haya kwa nafsi yake tu alikuwa amepokea maelekezo kutoka kwa Bwana anasema na yakuwa nimefanya haya kwa neno lako, alikuwa ameutafuta uso wa Mungu kwa kiwango cha kutosha ili Mungu aweze kuthibitika na sio Mungu tu na nabii wa kweli aweze kuthibitika, Mungu anapojibu kwa Moto utendaji wake huonekana kwa Dhahiri na hiki ndicho kilichotokea watu wote walijua kuwa Mungu wa Ibrahimu, na Isaka na Yakobo kuwa ni Mungu wa kweli, na hapo ndipo Eliya na watu wote walipokuwa na nguvu dhidi ya manabii wa uongo, kanisa la Mungu leo tutaweza kuwashinda manabii wa uongo ikiwa tu miujiza yetu, itazidi yao, Imani yetu itazidi yao, makusanyiko yetu yatazidi yao, watu wenye changamoto mbalimbali duniani watatujia na kuhitaji msaada kutoka kwetu, hakuna siasa kwa Mungu, Mungu wa kweli atadhihirika na mashaka ya watu yataondoka ikiwa tu tutakuwa na uwezo wa kujibu changamoto zinazowakabili watu, hatuwezi kamwe kumtanganza Mungu kwa ujasiri endapo Mungu wetu hawezi kuwasaidia watu hata ugonjwa wa mafua tu, Umefika wakati tumtafute Bwana, tumtake Bwana na nguvu zake ili Mungu wetu aweze kudhihirika wazi wazi kwa wale wasioamini na wale wanaotupinga hivi ndivyo Eliya alivyoibuka mbabe mbele ya wale waliokuwa wanampinga yaani Mungu wake kuonyesha uwezo wa kujibu kwa moto na hii ndio tofauti ya Mungu aliye hai na mungu aliyekufa.

Mwisho wa Manabii wa uongo

Jambo kubwa la msingi lililotokea ni kuwa manabii wa uongo walipoteza washirika wao kwani watu wote baada ya tukio hilo walimrudia Mungu, Walitambua kuwa Mungu wa Ibrahimu, na Isaka na Yakobo, Mungu wa Eliya ni Mungu wa kweli na walitubu wakitambua ya kuwa wamefanya dhambi kwa kuabudu miungu mingine 

1Wafalme 18:39 “Na watu wote walipoona, wakaanguka kifudifudi; wakasema, Bwana ndiye Mungu, Bwana ndiye Mungu.

Ni lazima watu wote duniani wamjue Mungu wa kweli, zimekuweko falsafa nyingi duniani na dini nyingi lakini watu wengi hawamjui Mungu wa kweli, sisi kama Eliya Leo hatuna budi kuitangazia jamii kuwa Yesu Kristo ndiye njia na kweli na uzima, Yeye ni ishara mashuri kwani amefufuka yu hai na ameketi mkono wa kuume wa Mungu baba Mwenyezi, watu wote wanapaswa kutambua hilo na kuacha mashaka na kusita sita wote wanapaswa kumchagua Mungu aliye hai na wa kweli kwa hiyo ni muhimu kwetu kufanya uamuzi leo, na kumkubali Yesu kuwa Bwana na mwokozi wa maisha yetu, watu wote wanapaswa kujua kuwa duniani kuna watu wengi wanaabudu, wengine mpaka wanajikata kata na kujitoa dhabihu, lakini hii haimaanishi kuwa jitihada zao za kidini na kiimani walizonazo kwamba zinaweza kuwaokoa au kana kwamba wako sahihi, wakati umefika na saa ipo ambayo waabuduo halisi watamuabudu Mungu katika Roho na kweli, na wakati huo ni sasa, ni lazima jamii itambue kuwa kubudu kusiko sahihi kuna matokeo yasiyo sahihi na moja ya matukio hayo ni kutupwa katika ziwa liwakalo Moto, Mungu sio tu awawahukumu manabii wa uongo lakini pia ataihukumu miungu kwa sababu imeiba utukufu wake kwa muda mrefu na kwa miaka Mingi,  na kuwapotosha wanadamu. Jamii ya watu wa wakati wa Eliya walirudisha utukufu kwa Mungu wakisema Bwana ndiye Mungu, Bwana ndiye Mungu, Navutiwa na maneno hayo ninapoyasoma katika Biblia ya kingereza iitwayo Complete Jewish Bible “CJB” inasoma hivi 

When all people saw it, they fell on their faces and said, ADONAI is God! ADONAI is God."

Watu walisujudu na kukubali kuwa Mungu ndiye Bwana Mungu ndiye Bwana, watu walirudisha utii kwa Mungu na huo ndio ukawa mwisho wa manabii wa uongo, hatuwezi kuwaua leo manabii wa uwongo, lakini nyakati za agano la kale watu makafiri waliuawa hivyo Eliya aliamuru manabii wa baali wakamatwe na wakachinjwa, sisi namna yetu ya kuwachinja ni kumuhubiri Mungu wa kweli na kufanya miujiza na ishara za kweli kwa jina la Yesu Kristo, kwa kusudi la kurejesha mioyo ya watu kwa Mungu wa kweli na kumpa yeye heshima na utukufu, huku wakitambua kuwa Yesu ndiye njia na kweli na uzima!

1Wafalme 18:40 “Eliya akawaambia, Wakamateni hao manabii wa Baali, asiokoke hata mmoja. Wakawakamata; na Eliya akawachukua mpaka kijito cha Kishoni, akawaua huko.

Hitimisho 

Kumbuka kumtumikia Mungu wa kweli, kumbuka kumuabudu Mungu wa kweli na ondoka katika kusita sita, acha kupeleka ibada mahali kusiko sahihi, je umewahi kujiuliza kama unaabudu Mungu wa kweli? Kama uko kwenye Imani sahihi au la? Amua leo kabla ya hukumu 

Mwenye haki ataishi kwa Imani akisitasita Roho yangu haina furaha naye asema Bwana

Na. Rev. Innocent Samuel Kamote

Mkuu wa wajenzi mwenye Hekima.  

Jumatano, 15 Januari 2025

Kutoka Misri Nalimwita Mwanangu!


Mathayo 2:13-15 “Na hao walipokwisha kwenda zao, tazama, malaika wa Bwana alimtokea Yusufu katika ndoto, akasema, Ondoka, umchukue mtoto na mama yake, ukimbilie Misri, ukae huko hata nikuambie; kwa maana Herode anataka kumtafuta mtoto amwangamize. Akaondoka akamchukua mtoto na mama yake usiku, akaenda zake Misri; akakaa huko hata alipokufa Herode; ili litimie neno lililonenwa na Bwana kwa ujumbe wa nabii, akisema, Kutoka Misri nalimwita mwanangu.”

 


Utangulizi:

Ni muhimu kufahamu kuwa Taifa la Misri ni moja ya mataifa muhimu sana katika historia nzima ya ukombozi wa mwanadamu na Israel, Taifa la Misri limetumiwa na Mungu katika maandiko kutufundisha maswala makuu kadhaa muhimu na penginepo unaweza kuongezea na mengine, lakini Misri ni alama ya Usalama kwa watu wa Mungu, Lakini Misri pia inasimama kama alama ya utumwa na mateso kwa watu wa Mungu na pia, Misri inasimama kama alama uhamisho kwa watu wa Mungu, na sehemu ya alama ya ukatili kwa watoto wa Mungu, Kwa hiyo Misri ni moja ya taifa ambalo Mungu amelitumia kama Ishara ya ukombozi  na katika kutupa somo watu wake, Hakuna sababu ya kuichukia Misri kama vile ni sehemu mbaya na badala yake tunaweza kuipenda Misri kama sehemu muhimu ya ardhi iliyotumiwa na Mungu kutufundisha maswala kadhaa muhimu katika maisha.

Mwanzo 12:10 “Basi kulikuwa njaa katika nchi ile; Abramu akashuka Misri, akae huko kwa muda maana njaa ilikuwa nzito katika nchi.”

Tunaona kuwa wakati ambapo kulikuwa na njaa katika nchi ya Kanaani, Ibrahimu alishuka Misri kwa muda kwaajili ya kupisha njaa kali na nzito iliyokuwa imejitokeza Kanaani, kwa hiyo Misri hapa inaonekana kuwa ni eneo salama kwa Abramu na watu wake kwaajili ya Usalama wao, sio tu wakati wa Ibrahimu, lakini hata wakati wa Yakobo njaa kubwa ilipotokea wana wa Israel sio tu walishuka kununua nafaka Misri lakini kupitia Yusufu walishuka na kukaa Misri katika eneo la Gosheni wao pamoja na mifugo yao kwa kusudi la kupisha njaa kali iliyoikumba dunia ya wakati ule 

Mwanzo 47:27-30 “Israeli akakaa katika nchi ya Misri, katika nchi ya Gosheni. Wakapata mali humo, wakaongezeka na kuzidi sana.Yakobo akaishi katika nchi ya Misri miaka kumi na saba, basi siku za miaka ya maisha yake Yakobo ilikuwa miaka mia moja na arobaini na saba. Siku za kufa kwake Israeli zikakaribia; akamwita mwanawe Yusufu, akamwambia, Kama nimeona kibali machoni pako, weka mkono wako chini ya paja langu, ukanifanyie rehema na kweli; nakusihi usinizike katika Misri. Lakini nitakapolala pamoja na baba zangu, unichukue toka Misri, unizike katika kaburi lao. Akasema, Nitafanya kama ulivyosema.” 

Kwa hiyo tunajifunza hapo kuwa Misri ilifanyika mahali salama kwaajili ya Ibrahimu, na baadaye Yakobo na wana wa Israel kabla ya utawala uliokuja baadaye na kuwageuza Israel kuwa watumwa, na sasa katika namna ya kushangaza tunaiona Misri sasa ikiwa alama ya Usalama kwa Yusufu na Mariamu na mtoto Yesu pale alipokuwa anawindwa na Herode kwa kusudi la kutaka kumwangamiza

Mathayo 2:13-15 “Na hao walipokwisha kwenda zao, tazama, malaika wa Bwana alimtokea Yusufu katika ndoto, akasema, Ondoka, umchukue mtoto na mama yake, ukimbilie Misri, ukae huko hata nikuambie; kwa maana Herode anataka kumtafuta mtoto amwangamize. Akaondoka akamchukua mtoto na mama yake usiku, akaenda zake Misri; akakaa huko hata alipokufa Herode; ili litimie neno lililonenwa na Bwana kwa ujumbe wa nabii, akisema, Kutoka Misri nalimwita mwanangu.”

Kwa hiyo Misri ni sehemu salama, ni alama ya usalama, lakini vile vile Misri ni alama ya utumwa na ukatili, Misri vile vile ni alama ya uhamishoni, Misri haikuwa nchi ya ahadi, lakini ilikuwa ni sehemu Muhimu sana kwa Usalama wa Israel, uhifadhi wao, maendeleo yao, uimara wao na Ustawi wao, kwa hiyo Misri ina historia kubwa sana katika fundisho la ukombozi wa mwanadamu na wana wa Israel, na zaidi sasa kwa Usalama wa Yesu Kristo aliye mwokozi wa ulimwengu.

Leo tutachukua Muda kiasi kujifunza juu ya somo hili muhimu katika msimu unaoelekea sikukuu za kuzaliwa kwa Mwokozi, kwa kutafakari ujumbe huu wenye kichwa Kutoka Misri Nalimwita Mwanangu na tutajifunza somo hili kutoka Misri nalimwita Mwanangu kwa kuzingatia vipengele viwili tu vifuatavyo:-


Kutimizwa kwa neno lililonenwa na Bwana 

Kutoka Misri Nalimwita mwanangu



Kutimizwa kwa neno lililonenwa na Bwana.

Mathayo 2:13-15 “Na hao walipokwisha kwenda zao, tazama, malaika wa Bwana alimtokea Yusufu katika ndoto, akasema, Ondoka, umchukue mtoto na mama yake, ukimbilie Misri, ukae huko hata nikuambie; kwa maana Herode anataka kumtafuta mtoto amwangamize. Akaondoka akamchukua mtoto na mama yake usiku, akaenda zake Misri; akakaa huko hata alipokufa Herode; ili litimie neno lililonenwa na Bwana kwa ujumbe wa nabii, akisema, Kutoka Misri nalimwita mwanangu.”

Kitendo cha Malaika wa Bwana kumtokea Yusufu katika ndoto na kumuelekeza kumchukua mtoto na Mariamu mama yake kisha waelekee Misri, ni swala linalozingatia Usalama wa Yesu kule Misri, kwa sababu kulikuwa na hatari ya kutaka kuuawa kwa mtoto huyu kutoka kwa mfalme Herode, na Baada ya kifo cha Herode Bwana alimtokea Tena Yusufu na kumtaka arejee Israel, lakini katika mtazamo wa Matayo yeye analiona tukio hili ni kutimizwa kwa unabii wa mjumbe wa Bwana yaani nabii Hosea aliyesema haya katika 

Hosea 11:1 “Israeli alipokuwa mtoto, nalikuwa nikimpenda, nikamwita mwanangu atoke Misri.” 

Kimsingi Nabii Hosea anaonyesha jinsi Mungu alivyoipenda Israel na kuwaita kuja katika nchi ya Mkanaani, Mathayo anamuona nabii Hosea kuwa anazungumza kihistoria na kinabii, kihistoria nabii Hosea anazungumzia tukio la Mungu kuwaokoa wana wa Israel watoke uhamishoni, watoke katika nchi ya makimbilio na kuwarejeza katika nchi ya ahadi, Mungu alifanya hivyo kwa upendo wake, kwa watu wake akiwa amewabariki na kuwaimarisha kijeshi na kisayansi na kuwafunza sheria na taratibu zake, Israel ni watoto wa Mungu ni watoto wake aliowachagua nimzaliwa wake wa kwanza 

Kutoka 4:22 -23 “Nawe umwambie Farao, BWANA asema hivi, Israeli ni mwanangu mimi, mzaliwa wa kwanza wangu; nami nimekuambia, Mpe mwanangu ruhusa aende, ili apate kunitumikia, nawe umekataa kumpa ruhusa aende; angalia basi, mimi nitamwua mwanao, mzaliwa wa kwanza wako.” 

Lakini kinabii Mathayo anauona ujumbe wa Hosea kuwa unamzungumzia Yesu Kristo, nikamwita mwanangu atoke Misri, Mathayo anamuona Yesu kuwa ndiye Israel Halisi na kuwa wengine wote ni kama wamekuwa Israel mwitu, hii ni kwa sababu Israel walipopandishwa katika nchi ya ahadi Mungu alitarajia wangemtii yeye na kuacha kuabudu miungu mingine lakini hata hivyo mwanzoni walishindwa na ni Yesu Peke yake aliyeweza kutii maagizo yote ya Mungu na kuitimiza Sheria Yote hivyo Mathayo anakubaliana na maandiko kuwa Yesu ndiye Israel halisi na ndiye mzabibu wa kweli  

Yeremia 2:21 “Nami nalikuwa nimekupanda, mzabibu mwema sana, mbegu nzuri kabisa; umegeukaje, basi, kuwa mche usiofaa wa mzabibu-mwitu machoni pangu? ” 

Yohana 15:1-2 “Mimi ndimi mzabibu wa kweli, na Baba yangu ndiye mkulima. Kila tawi ndani yangu lisilozaa huliondoa; na kila tawi lizaalo hulisafisha, ili lizidi kuzaa.”

kwa msingi huo maneno haya kutoka Misri nalimwita mwanangu katika mtazamo wa kinabii Mathayo anauona kuwa unabii huu unatimizwa kwa Yesu Kristo, Lakini pia ni wito kwa watoto wote wa Mungu kuondoka katika inchi isiyo sahihi na mahali pasipo sahihi, na kujiweka wakfu kwaajili ya kumtumikia Mungu aliye hai.Mungu hafurahii hata kidogo uwepo ugenini, ukimbizini, na utumwani

Kutoka Misri nalimwita mwanangu.

Tumejifunza katika utangulizi ya kuwa Misri inawakilisha maswala mbalimbali ikiwa ni pamoja na utumwa na ukatili, Japo Mungu pia aliitumia Misri kuwaneemaesha Israel na kumtunza Musa na Yusufu na Ibrahimu na Yesu, Hata hivyo Kimsingi ujumbe huu wa kutoka misri nalimwita mwanangu haukuwa tu unamuhusu Israel na Yesu pekee, lakini ni ujumbe wa Mungu leo kwa watu wake wote walioko uhamishoni, Mungu anakuita utoke katika hali yoyote ya mashaka, wasiwasi, kupoteza tumaini na kuishi kama mkimbizi, Mungu anataka urudi katika uhalisia wako Misri haikuwa nchi halisi ya Israel wala haikuwa nchi halisi ya Yesu, ilikuwa ni sehemu tu ya kujihifadhi, sasa Mungu anakuita katika eneo lako la asili, Eneo ambalo amekusudia kukupumzisha, eneo ambalo amekusudia kukupa raha, eneo ambalo amekusudia kukutumia eneo ambalo amekusudia kukupa utulivu, Eneo ambako ameandaaa ustawi wako na makazi yako ya kudumu!, hapo ulipo uko kwenye nchi ya utumwa, uko uhamishoni, uko unatumikishwa, uko na mizigo, uko ukimbizini,huko huwezi kumuabudu Mungu kwa uhuru, na sasa Bwana kwa kinywa cha nabii anakuita wewe ni mtoto wake halisi na hauko mahali halisi alikokuweka anataka akutoe huko, kutoka Misri nalimwita mwanangu! Mungu hatakubali uendelee kuweko uhamishoni, Mungu hawezi kukubali mtoto wake aendelee kuwepo Misri ni lazima atakuita kutoka huko, Hosea analiona tukio hilo kana kwamba Mungu aliwaita wana wa Israel watoke Misri na Mathayo analiona tukio hilo kuwa Mungu alimuita Yesu kutoka Misri nami naliona tukio hilo kuwa Mungu anakuita wewe Katika nafasi aliyokukusudia kwayo. Kwa sababu

Kutoka Misri  ni kujitenga kwaajili ya Mungu ili umuabudu na kumtumikia yeye na sio Farao, Mungu anajua ya kuwa huwezi kumuabudu Mungu kwa uhusu na Amani ukiwa Misri, Farao atataka uendelee kuwako Misri ili utumie muda mwingi kumtumikia yeye kuliko Mungu wako, au umuabudu Mungu pamoja na machukizo ya dhambi za ulimwengu

Kutoka 8:25-26. “Farao akawaita Musa na Haruni akawaambia, Endeni mkamtolee Mungu wenu dhabihu ndani ya nchi hii. Musa akasema, Haitupasi kufanya hivyo; kwa kuwa tutamchinjia sadaka BWANA, Mungu wetu, na hayo machukizo ya Wamisri; je! Tutachinja sadaka ya hayo machukizo ya Wamisri mbele ya macho yao, wasitupige kwa mawe? ” 

Farao hatatamani uende mbali na Misri kwa sababu hataki uzame sana katika uhusiano wako na Mungu anatamani uwe vuguvugu, anatamani uishi maisha mchanganyiko, hataki uwe mbali na changamoto zake za kitumwa na ukawe huru kwa Mungu na ndio maana Mungu anatoa wito utoke Misri, na kuja katika inchi sahihi ambako utasitawi, kiroho, kimwili na nasfi yako kuburudika 

Kutoka 8:27-28 “La, tutakwenda safari ya siku tatu jangwani, tumchinjie dhabihu BWANA, Mungu wetu, kama atakavyotuagiza. Farao akasema, Mimi nitawapa ruhusa mwende, ili mmchinjie dhabihu BWANA, Mungu wenu, jangwani; lakini hamtakwenda mbali sana; haya niombeeni.”

Misri itatamani wanaume tu waende, lakini wanawake na watoto wabaki, Mungu anataka wote wanaume na familia zao wote wamjue Mungu, ukiwa Misri farao atatamani wanaume tu ndio wamuabudu Mungu wao peke yako bila kujali familia zetu, Musa hakukubali alisema tutakwenda kumuabudu Mungu na kila kitu tulicho nacho na hakutasalia hata ukwato

Kutoka 10:9-11 “Musa akamjibu, Tutakwenda na vijana wetu na wazee wetu, na wana wetu, na binti zetu, tutakwenda na kondoo zetu na ng'ombe zetu; kwa kuwa inatupasa kumfanyia BWANA sikukuu. Lakini akawaambia, Ehe, BWANA na awe pamoja nanyi, kama nitakavyowapa ruhusa kwenda zenu pamoja na watoto wenu; angalieni, kwa kuwa pana uovu huko mbele yenu. Sivyo; endeni ninyi mlio watu wazima, mkamtumikie BWANA; kwa kuwa ndilo jambo mtakalo. Nao walifukuzwa usoni pa Farao.”

Misri itatamani uondoke mikono mitupu, usiwe na mali, Misri ianataka mali zote zibaki, mapato yako yote na kila kitru ukipendacho kibaki kwaajili ya uchumi wa Misri na haitataka uende na kitu kwa Mungu wala kutumia mapato yako na mali zako kwa utukufu wa Mungu na ndio Maana Mungu anakuita utoke Misri ili kila alichikubariki na kukupa kitumike kwaajili ya utukufu wa Mungu

Kutoka 10:24-26 “Farao akamwita Musa, na kumwambia, Haya, nendeni, mkamtumikie BWANA; kondoo zenu na ng'ombe zenu tu na waachwe; watoto wenu nao na waende pamoja nanyi. Musa akasema, Ni lazima utupe mikononi mwetu na wanyama wa dhabihu na wa sadaka za kuteketezwa, ili tupate kumchinjia BWANA Mungu wetu dhabihu. Makundi yetu pia watakwenda pamoja nasi; hautasalia nyuma hata ukwato mmoja; kwa maana inampasa kutwaa katika hao tupate kumtumikia BWANA, Mungu wetu; nasi hatujui, hata tutakapofika huko, ni kitu gani ambacho kwa hicho inatupasa kumtumikia BWANA.

Kimsingi Mungu aliwaita watu wake watoke Misri ili wamuabudu yeye kwa uhuru na pasipo hofu, wamtumikie yeye na sio kuwa chini ya nira mbili, yaani sio kuwa chini ya utumwa wa dunia na utumishi wa Mungu, kuitwa kuja kutoka Misri ni kutengwa kwaajili ya utumishi ambao Mungu ameukusudia, ni kutengwa kwaajili ya kazi yake, ni kurejeshwa katika eneo sahihi, umuabudu yeye peke yake 

Na. Rev. Mkombozi Samuel Kamote

Mkuu wa Wajenzi mwenye Hekima!

Jumanne, 7 Januari 2025

Msimwite Mtu Baba Duniani!


Mathayo 23:8-10 “Bali ninyi msiitwe Rabi, maana mwalimu wenu ni mmoja, nanyi nyote ni ndugu. Wala msimwite mtu baba duniani; maana Baba yenu ni mmoja, aliye wa mbinguni. Wala msiitwe viongozi; maana kiongozi wenu ni mmoja, naye ndiye Kristo.




Utangulizi:

Moja ya maonyo aliyoyatoa Yesu Kristo Kiongozi mkuu wa wokovu wetu kwa wanafunzi wake ni pamoja na kuacha kutafuta heshima kutoka kwa wanadamu na au kuwapa wanadamu heshima isiyostahili, Yesu aliwakumbusha wanafunzi wake kuwa wao ni ndugu, yaani kaka na dada katika Bwana, kwa hivyo wakristo ni familia moja ya Mungu, na Mungu pekee ndiye baba yetu,  lakini zaidi ya yote aliwaonya wasimuite mtu rabi wala baba duniani wala kiongozi, kwa kuwa baba yetu ni mmoja aliye wa mbinguni na Mwalimu wetu ni mmoja ndiye Yesu na wala tusiitwe viongozi, kwa hiyo kamwe hatupaswi kutafuta heshima, wala kumpa mtu heshima ambayo hastahili na badala yake kuhakikisha tunawatumikia watu,  na kuwa heshima na utukufu ni mali ya Mungu Baba yetu.

Marko 10:42-45 “Yesu akawaita, akawaambia, Mwajua ya kuwa wale wanaohesabiwa kuwa wakuu wa Mataifa huwatawala kwa nguvu, na wakubwa wao huwatumikisha. Lakini haitakuwa hivyo kwenu; bali mtu anayetaka kuwa mkubwa kwenu, atakuwa mtumishi wenu, na mtu anayetaka kuwa wa kwanza wenu, atakuwa mtumwa wa wote. Kwa maana Mwana wa Adamu naye hakuja kutumikiwa, bali kutumika, na kutoa nafsi yake iwe fidia ya wengi.”

Mafundisho ya Yesu Kristo ni tofauti sana na mafundisho ya ulimwengu huu, watu wa ulimwengu huu wanatafuta kutambulika, wanatafuta umaarufu na heshima kubwa na kutawala, na kutumikisha au kutumikiwa,lakini Kristo anasisitiza unyenyekevu, kujishusha na kuwatumikia watu, na wale wanaojinyenyekeza wawapo duniani watainuliwa katika ufalme wa Mungu, Leo tutachukua muda sasa kujifunza kwa kina na mapana na marefu somo hili zuri lenye na lenye mabishano makubwa sana lenye kichwa“Msimwite mtu Baba duniani” kwa kuzingatia vipengele viwili vifuatavyo:-


Asili na matumizi ya neno Baba.

Msimwite Mtu Baba Duniani!. 


Asili na matumizi ya neno Baba.

Ni muhimu kufahamu kuwa itakuwa ni vigumu sana kuelewa kwanini Yesu anawaonya wanafunzi wake wasimwite mtu Baba hapa duniani, kama hatutaelewa kuwa katika Biblia yaani neno la Mungu jina hilo baba lilikuwa lina maana gani, na lilikuwa linatumikaje hususani katika tamaduni za kiebrania, ni muhimu kufahamu kuwa:- 

Neno baba katika lugha ya asili ya Kiebrania linatumika kama neno “Abh” “abea” au “av” na katika Kiyunani ni “Patēr” kwa kiingereza “Father” na katika lugha ya kiaram ni “Abba” ambalo maana yake ni mtu anayeaanzisha jambo ambalo anafikiri kuwa ni sahihi na anahakikisha linaendelea kuwepo, Baba ni mmiliki, Baba ni Mwanzilishi, Baba ni Mlinzi, Mzazi wa kiume, Baba ni mwenye mamlaka ya uzima au kifo, Baba ni muheshimiwa. (Upholder, the owner, Founder, Protector, A male ancestor, Respect). Katika maandiko yaani nyakati za agano la kale na agano jipya pia Neno baba lilipotumika liligusa maeneo hayo muhimu katika maneno hayo niliyoyataja hapo juu. Lakini neno la kiaramu “Abba” linahusika na uhusiano wa ndani zaidi wa kifamilia sawa na neno “Papa” au “Daddy” Hebu sasa tuchukue muda wa kutosha kuangalia jinsi neno Baba lilivyokuwa likitumika katika maandiko:-

Mzazi au mlezi wa kiume  “Abh”– Jina baba au neno baba katika tamaduni za kiebrania na warumi lilikuwa lina uhusiano wa moja kwa moja na Mzazi mwanaume ambaye ana uhusiano wa damu au uhusiano wa kibailojia wa moja kwa moja na wahusika kama ni watoto wa kiume au wa kike, kwa hiyo matumizi ya neno baba yalimaanisha moja kwa moja baba mzazi, mwanaume ambaye anahusika kukuzaa kibaiolojia kama mzazi wa damu, na hata babu yako na babu yake baba yako nao waliweza kuunganishwa katika kundi hilo kumaanisha baba zako yaani watu ambao ni sababu ya wewe kuwepo duniani, ni waanzilishi wa asili yako ya kimwili duniani, ni sababu ya wewe kuweko kwako duniani, ni damu yako, hawa Mungu anawatambua na ameamuru waheshimiwe na kuna Baraka za kufanya hivyo ikiwa ni pamoja na kupewa siku nyingi za kuishi na heri duniani, Kimsingi hawa ukiwaita baba hakuna shida na Yesu hakukataza tukio la aina hii kwa sababu hii ni kawaida na mzazi au mlezi wa familia yako anastahili heshima hii, kwa hiyo hakuna dhambi wala kosa kumuita mzazi wako baba hii ni heshima yake na ni agizo la Mungu katika maandiko kuwa wazazi wetu wanastahili kuheshimiwa. Kwa hiyo matumizi baba kwa mtu aliyekuzaa au kukulea hayana shida katika katazo la Yesu Kristo.


Kutoka 20:12 “Waheshimu baba yako na mama yako; siku zako zipate kuwa nyingi katika nchi upewayo na BWANA, Mungu wako.” (Neno linalotumika hapo ni âb au av)


Matendo 7:32 “Mimi ni Mungu wa baba zako, Mungu wa Ibrahimu, na Mungu wa Isaka, na Mungu wa Yakobo. Musa akatetemeka, asithubutu kutazama.” (Neno linalotumika hapa ni Patēr au Patriachs)


1Wafalme 11:42-43 “Na siku alizotawala Sulemani katika Yerusalemu juu ya Israeli wote zilikuwa miaka arobaini. Naye Sulemani akalala na baba zake, akazikwa katika mji wa Daudi baba yake; na Rehoboamu mwanawe akatawala mahali pake.” (Neno linalotumika hapa ni âb au av)


Mababa hawa wa duniani wana mamlaka nyingi, ikiwa ni pamoja na kukuzaa, kukulea, kukupa elimu, kukupa chakula, kukutoa uoe au uolewe, kukulinda, kukuongoza, kukutia moyo, kukuelimisha, kukufundisha, pamoja na kukurithisha, Baba wa waabudu miungu zamani  walikuwa na mamlaka ya kuwatoa watoto wao kafara kwa miungu hivyo kuonyesha kuwa baba wa kibaiolojia pia alikuwa ana mamlaka ya uhai wako na kifo chako, Sawa tu na Ibrahimu alivyotaka kumtoa Isaka, au Yeftha alivyomtoa binti yake, hii ni mamlaka nzito sana aliyo nayo baba, Baba hawa wanaweza kukuonya, kukukemea, kukudekeza, kukuadhibu, kukufundisha hekima, kukurithisha Imani, kushughulika na mahitaji yako kukuhurumia  na hata kuwa rafiki na kadhalika. hawa ni baba wa miili yetu. Ni mababa wa kibaiolojia hawa wana haki ya kuitwa Baba. Kuitwa baba ni heshima yao maalumu na wala sio ya kuitafuta wamepewa na Mungu, kwa hiyo baba hawa huitwa baba wa miili yetu, na Mungu ni baba wa roho zetu. Unaweza kuona:-


Waebrania 12:7-9 “Ni kwa ajili ya kurudiwa mwastahimili; Mungu awatendea kama wana; maana ni mwana yupi asiyerudiwa na babaye? Basi kama mkiwa hamna kurudiwa, ambako ni fungu la wote, ndipo mmekuwa wana wa haramu ninyi, wala si wana wa halali. Na pamoja na hayo tulikuwa na baba zetu wa mwili walioturudi, nasi tukawastahi; basi si afadhali sana kujitia chini ya Baba wa roho zetu na kuishi? ” 


Zaburi 103:13 “Kama vile baba awahurumiavyo watoto wake, Ndivyo Bwana anavyowahurumia wamchao.


Kwa hiyo maana ya kwanza ya neno baba ni mzazi wa kiume aliyekuzaa au aliyekulea na kuku-kuza, baba ambaye mna asili ya damu na hata yule anayeweza kukuasili ili uwe mwanaye na kadhalika na wale waliohusika katika malezi yako baba mlezi hii ni kawaida. Na hao wanastahili kuitwa baba lakini ni baba wa miili yetu na kwa habari za kiroho, Mungu ndiye baba yetu, anaitwa Baba wa roho zetu unaweza kuona!.


Mwanzilishi – Jina au neno baba pia katika maandiko linatumika kumuelezea mwanzilishi au aliyeweka msingi wa jambo Fulani, aidha kiulimwengu, au kitaifa, au kiimani, au kitabia au kifalsafa au kuweka miongozo, kwa hiyo waanzilishi wa kitu fulani au jambo Fulani au hata waanzilishi wa taifa, katika maandiko waliitwa baba wa hicho alichokianzisha yaani mgunduzi, au mwanzilishi au  sababu au chanzo cha hiyo tabia au jambo, mwanzilishi au mgunduzi wa jambo fulani linaweza kuwa jema au baya hapa duniani  huyo naye katika maandiko aliitwa baba mfano:-


ImaniWarumi 4:11-12. “Naye aliipokea dalili hii ya kutahiriwa, muhuri ya ile haki ya imani aliyokuwa nayo kabla hajatahiriwa; apate kuwa BABA YAO WOTE WAAMINIO, ijapokuwa hawakutahiriwa, ili na wao pia wahesabiwe haki; tena awe baba ya kutahiriwa, kwa wale ambao si waliotahiriwa tu, bali pia wanazifuata nyayo za imani yake baba yetu Ibrahimu aliyokuwa nayo kabla hajatahiriwa.


Ibrahimu anaitwa baba wa Imani, kwa sababu ndiye mtu wa kwanza kuwasiliana na Mungu aliye hai baada ya miaka mingi sana tangu nyakati za Nuhu, na hivyo kuwa sababu ya watu wengi kumwamini Mungu na kumjua Mungu aliye hai na imani kubwa duniani zikiwemo ya kiyahudi, kikristo na nyinginezo ambazo mzizi wake ni nabii Ibrahimu zinakubali na zinamtambua Ibrahimu kama baba wa Imani yaani mwanzilishi wa Imani yetu kwa Mungu na ndiye mgunduzi wa uhusiano na Mungu wa kweli duniani.


Uongo na dhambiYohana 8:44 “Ninyi ni wa baba yenu, Ibilisi, na tamaa za baba yenu ndizo mpendazo kuzitenda. Yeye alikuwa mwuaji tangu mwanzo; wala hakusimama katika kweli, kwa kuwa hamna hiyo kweli ndani yake. Asemapo uongo, husema yaliyo yake mwenyewe; kwa sababu yeye ni mwongo, na baba wa huo.”


Hapa shetani anatajwa kama baba wa uongo, na mwanzilishi wa uongo duniani, ambaye hakuna kweli ndani yake yeye ni mwongo na baba wa huo, yaani shetani ndiye asili au mwanzilishi wa uongo, kwa hiyo neno baba hapa linatumika kuonyesha chanzo, asili au mwanzilishi, mwanzilishi wa uongo ni baba wa huo uongo.

 

Mgunduzi, au mwanzilishi (Meyased) – Mwanzo 4:20-22 “Ada akamzaa Yabali; huyo ndiye baba yao wakaao katika hema na kufuga wanyama. Na jina la nduguye aliitwa Yubali; huyo ndiye baba yao wapigao kinubi na filimbi. Sila naye akamzaa Tubal-kaini, mfua kila chombo cha kukatia, cha shaba na cha chuma; na umbu lake Tubal-kaini alikuwa Naama.” 


Hapa Yabali anatajwa kama asili au mwanzilishi wa kukaa katika mahema na kufuga wanyama, na Yubali ni mwanzilishi wa wapiga muziki yaani kinubi na filimbi, na Tubal-Kaini yeye ni mwanzilishi au mgunduzi wa vyombo vya kukatia vya chuma na shaba au mgunduzi wa silaha 


Aidha katika hali ya isiyokuwa ya kawaida Marekani walimuita George Washington na Abraham Lincoln kama Baba labda kwa sababu ya Washington kuwa mwanzilishi wa taifa hilo, na Lincoln kuwa mtu muhimu katika kujinga Marekani iliyotulia, India walimuita Mahatma Ghand, na Tanzania Mwalimu Nyerere kuwa baba wa mataifa yao, heshima hii kamwe hawajawahi kujipa wala kujiita wenyewe, lakini watu waliwaita hivyo kwa sababu labda ni waanzilishi wa mataifa yao, hatupati kuungwa mkono moja kwa moja kutoka katika maandiko kama wanaweza kufaa kuitwa hivyo kama waanzilishi.  


Uhusiano wa karibu na kihisia – katika tamaduni za kiebrania pia kama mtu alikuwa na uhusiano wa karibu sana na wewe wa kawaida na wa kihisia, waliweza pia kutumia neno baba, watu hawa sio tu walikuwa na uhusiano wa kihisia bali pia uhusiano wa uaminifu ambao unahusisha kujitoa na kushika ahadi na mwenye kumtunza mtu kwa ndani sana Neno la kiebrania linalotumika hapo ni “Masculine” maneno mengine yanayotumika kuelezea aina hii ya uhusiano wa kibaba ni Khesed – anayekutunza, Ahav - anayekupenda, Kesher – zaidi ya rafiki, Kirvah mnayetofautiana kiumri na Yada – unayemjua au unayemuingilia kimwili, hii hutumiwa sana na wanawake kuwaita waume zao baba, Paulo mtume alikuwa na uhusiano wa karibu na kanisa la Korintho na uhusiano wa kihisia kwa hiyo alitumia neno baba hapa kama mtu anayejali na kulilinda kanisa kwaajili ya mafundisho sahihi, na alimuita Timotheo mwanaye katika picha ya uhusiano kama huo, ukaribu na ufahamu wa kile anachiokifundisha zaidi.


1Wakorintho 4:15-17 “Kwa kuwa ijapokuwa mna waalimu kumi elfu katika Kristo, walakini hamna baba wengi. Maana mimi ndimi niliyewazaa katika Kristo Yesu kwa njia ya Injili. Basi, nawasihi mnifuate mimi. Kwa sababu hii nimemtuma Timotheo kwenu, aliye mwanangu mpendwa, mwaminifu katika Bwana, atakayewakumbusha njia zangu zilizo katika Kristo, kama vile nifundishavyo kila mahali katika kila kanisa.”


Paulo mtume alikuwa ndiye mwanzilishi wa kanisa la Korintho na aliwazaa watoto wa kiroho kupitia injili, na aliruhusu walimu wengine kutoka sehemu mbalimbali kufundisha katika kanisa la Korintho, lakini kutokana na uchungu aliokuwa nao na kutokana na kuwepo kwa walimu wa uongo aliwasihi wao kumfuata yeye kama anavyomfuata Kristo, na ama kumfuata Timotheo ambaye ni mwanae mwaminifu katika bwana, hii ilikuwa lugha ya kisamiati yenye lengo la kutaka kuweka wazi kwa wakorintho namna na jinsi wanavyotakiwa kupokea mafundisho kwa walimu wote lakini wakisheshimu mafundisho ya Msingi ya mwanzilishi wa kanisa hilo na kijana wake, lakini kielelezo ikiwa ni kama wanavyomfuata Kristo, hapa hapakua na agizo endelevu la Paulo kuitwa Baba, hivyo hajapingana Bwana.


Kwa hiyo neno kla kiebrania pia meyased linafaa kutumika hapa kama mwanzilishi, mwanzilishi wa kanisa la Korintho, kwa kiyunani megiasménos, yaani kuwazaa kwa njia ya nguvu za Mungu (injili) wao kuwa kanisa. Na katika uhusiano wa Paulo na Timotheo, Paulo alimuita Timotheo mwanae kwa sababu ya umri, malezi na namna alivyoshughulika na kijana huyu kwa uhusiano wa ndani sana hata kutahiriwa kwa Timotheo ona 


Matendo 16:1-3 “Basi akafika Derbe na Listra, na hapo palikuwa na mwanafunzi mmoja jina lake Timotheo, mwana wa mwanamke Myahudi aliyeamini; lakini babaye alikuwa Myunani. Mtu huyo alishuhudiwa vema na ndugu waliokaa Listra na Ikonio. Paulo akamtaka huyo afuatane naye, akamtwaa akamtahiri kwa ajili ya Wayahudi waliokuwako pande zile; kwa maana wote walijua ya kuwa babaye ni Myunani.” 


Paulo mtume alikuwa na uhusiano wa karibu na Timotheo, na hivyo alimuita mwanangu, hii ilikuwa ni katika kudumisha uhusiano waliokuwa nao binafsi “TEKNON” katika mandiko ya kiyunani uhusiano wa baba na mwanae, hii ilikuwa katika uhalisia wa huduma zao na sio kuwa Paulo alitafuta heshima au kuliagiza kanisa kumuite yeye Baba, wakati wote Paulo alijiita Mtumwa wa Yesu Kristo “Doulos” akimaanisha kuwa yeye ni mtumwa wa Yesu Kristo na sio baba kumbuka hilo, alijitoa maisha yake kutumikia na wala sio kutumikiwa kwa hiyo matumizi na ubaba hapa hayakumaanisha mitume waitwe baba.


Katika mahusiano hayo ya kiumri pia utaweza kumuonya mtume Yohana nadhani kwa sababu ya umri au utu uzima aliokuwanao yeye naye alikuwa akitumia lugha ya kuwaita washirika watoto, hii ni kwa sababu ya umri ona 


1Yohana 2:1 “Watoto wangu wadogo, nawaandikia haya ili kwamba msitende dhambi. Na kama mtu akitenda dhambi tunaye Mwombezi kwa Baba, Yesu Kristo mwenye haki, naye ndiye kipatanisho kwa dhambi zetu; wala si kwa dhambi zetu tu, bali na kwa dhambi za ulimwengu wote.”


Biblia ya kiingereza ya “Complete Jewish Bible” inatumia neno “Wanangu” yenyewe inasema hivi “My Children, Iam writing you these things so that you won’t sin. But if anyone does sin, we heve Yeshua the Messiah, the Tzaddik, who pleads our cause with the Father”


Muumba au kiini Adonai (Lord or Master) – Waefeso 1:17 “Mungu wa Bwana wetu Yesu Kristo, Baba wa utukufu, awape ninyi roho ya hekima na ya ufunuo katika kumjua yeye;”


Ayubu 38:28-29 “Je! Mvua ina baba? Au ni nani aliyeyazaa matone ya umande? Barafu ilitoka katika tumbo la nani? Na sakitu ya mbinguni ni nani aliyeizaa?


Neno baba pia linatumika kama neno Lord yaani Bwana mkubwa, na Master yaani Mwalimu au kwa kiibrania Adonai hii ikiwa na maana ya Bwana wa Mabwana, au Bwana wa viumbe vyote kwa hiyo huyu ni chanzo cha uhai wa kimwili na kiroho na hivyo neno Adonai bila shaka lina sifa ya kutumiwa kwa Mungu peke yake

Kiongozi wa kiroho au nabii – Nyakati za agano la kale kiongozi wa kiroho kama nabii aliitwa baba pia hii ni kabla ya katazo la Yesu Kristo wakati wa agano jipya, lakini waitaji walilia hivyo kutoka moyoni si kwa agizo la manabii kama ilivyo leo, lakini hii pia ilitokana na uhusiano wa karibu na kihisia, wakati mwingine sio wachungaji na watumishi wa Mungu wanaojiita baba na ndio maana agizo la Yesu Kristo linasisitiza “Msimwite mtu baba duniani”, hii maana yake nini inawahusu sana waitaji, manabii hata hivyo walikuwa wanyenyekevu na hawakuchukulia kuitwa baba kama heshima ya kuidai, lakini watu wa Mungu wenyewe kwa hiyari waliwaita baba, sasa tunalo katazo kutoka kwa Yesu Kristo Msimwite mtu baba duniani. 


2Wafalme 2:11-13 “Ikawa, walipokuwa wakiendelea mbele na kuongea, tazama! Kukatokea gari la moto, na farasi wa moto, likawatenga wale wawili; naye Eliya akapanda mbinguni kwa upepo wa kisulisuli. Naye Elisha akaona, akalia, Baba yangu, baba yangu, gari la Israeli na wapanda farasi wake! Asimwone tena kabisa; akashika mavazi yake mwenyewe, akayararua vipande viwili. Kisha akaliokota lile vazi la Eliya lililomwangukia, akarudi, akasimama katika ukingo wa Yordani.”


2Wafalme 13:14 “Basi Elisha alikuwa ameshikwa na ugonjwa wake uliomwua; naye Yehoashi mfalme wa Israeli akatelemka amtazame, akamlilia mbele yake, akasema, Baba yangu! Baba yangu! Gari la Israeli na wapanda farasi wake! ” 


Kuitwa baba kama tamaduni au mapokeo  -  Aidha Kanisa Catholic, Othodoxy, Anglican na Lutherran huwaita viongozi wao wa kidini Babakwa mujibu wa tamaduni zao au mapokeo yao, na madai yao makubwa ni ushirikiano au uhusiano wa karibu ulioko kati ya washirika na makuhani wa makanisa hayo wito huu ulipata nguvu katika karne za kati maarufu kama Middle Ages wakati wa utambuzi wa viongozi wa kiroho, kama makuhani Mapadre walipopewa heshima hii ya kuitwa baba na maaskofu wakiitwa Papa, watetezi wa hoja hii, ya kuwaita viongozi wa kiroho baba, wanamadai kuwa hata baadhi ya mitume waliitwa hivyo baba mfano


Yohana 2:1 “Watoto wangu wadogo, nawaandikia haya ili kwamba msitende dhambi. Na kama mtu akitenda dhambi tunaye Mwombezi kwa Baba, Yesu Kristo mwenye haki,”


1Timotheo 1:18 “Mwanangu Timotheo, nakukabidhi agizo hilo liwe akiba, kwa ajili ya maneno ya unabii yaliyotangulia juu yako, ili katika hayo uvipige vile vita vizuri;”


1Petro 5:12-13 “Kwa mkono wa Silwano, ndugu mwaminifu kama nionavyo, nimewaandikia kwa maneno machache, kuonya na kushuhudia ya kuwa hii ndiyo neema ya kweli ya Mungu. Simameni imara katika hiyo. Mwenzenu mteule hapa Babeli awasalimu, na Marko mwanangu.” 


Makanisa mengi leo ukiacha Catholic na Othodoxy wameanza kuwa na kusimika wanawake kuwa makasisi, Anglican na lutheran sasa siku hizi wana wachungaji wengi wanawake na makanisa mengi ya kipentekoste pia yamekuwa yakisimika makasisi wanawake, wachungaji wanawake n ahata kuwaruhusu kuhudumu na kuchunga makanisa wao wanaitwaje sasa katika heshima hii, tuwaite Mama, au tuwaite baba?  Utamaduni na mapokeo hapa yanasemaje Jibu la swali hilo unaweza kubaki nalo kichwani? 


Msimwite Mtu Baba Duniani! 

Yesu aliposema katika Mathayo 23:9 “Wala msimwite mtu baba duniani; maana Baba yenu ni mmoja, aliye wa mbinguni.” Alikuwa anazungumza moja kwa moja kwa wanafunzi wake na kinyume na waandishi yaani walimu waliobobea katika torati pamoja na mafarisayo yaani viongozi wa dini na baraza la Sanhedrin, kimsingi watu hawa walikuwa na tabia ya kujitukuza sana na kutafuta kuheshimiwa sana na watu wote, kuheshimiwa sio kubaya ni sehemu ya maagizo ya maandiko lakini walipenda sana kuheshimiwa na kutafuta umaarufu na heshima hiyo kwa nguvu na kimazingira, Baraza la wazee wakipenda kuitwa baba na waandishi wakipenda kuitwa Rabbi, kimsingi ndani yao hakukuwa na tabia ya unyenyekevu lakini walijawa na tamaa ya kutafuta heshima na waliitengenezea mazingira ya kuipata, mtu alikuwa asipowaita baba hawaridhiki na wanaweza kumuona kama anadharau, mioyoni mwao walijisikia heshima kubwa sana kuitwa baba, Rabbi na Viongozi na vichwa vilivimba, na Kimsingi Yesu alikuwa akiwaona mpaka nia ya ndani moyoni mwao na tabia zao

Marko 12:38-40 “Akawaambia katika mafundisho yake, Jihadharini na waandishi, wapendao kutembea wamevaa mavazi marefu, na kusalimiwa masokoni, na kuketi mbele katika masinagogi, na viti vya mbele katika karamu; ambao hula nyumba za wajane, na kwa unafiki husali sala ndefu; hawa watapata hukumu iliyo kubwa.”

Matendo 7:1-3 “Kuhani Mkuu akasema, Je! Mambo hayo ndivyo yalivyo? Naye akasema, Ndugu zangu na baba zangu, sikilizeni: Mungu wa utukufu alimtokea baba yetu Ibrahimu, alipokuwa katika Mesopotamia, kabla hajakaa Harani, akamwambia, Toka katika nchi yako na katika jamaa zako, ukaende hata nchi nitakayokuonyesha.”

Mafarisayo na Waandishi walipenda kuitwa Rabbi na Baba, na kila aina ya heshima ya hadharani ambako kimsingi wangeweza kuheshimika, walijifikiria wenyewe kuwa ni watu wa kuheshimika na ni walimu wakubwa na ndio maana Yesu alitumia nafasi hii kuwafundisha wanafunzi wake kuwa kinyume na tabia isiyo ya mfano ya kutafuta heshima, kama walivyo wao mafarisayo na sio hivyo tu aliwakataza wanafunzi wake kutokumuita mtu awaye yote Baba au Rabi,  Alisisitiza kuwa wakristo Mwalimu wao ni mmoja tu Bwana Yesu na baba yao ni Mmoja tu Baba wa mbinguni, tofauti na hilo wakristo wote ni ndugu, kaka na dada katika Bwana na wote ni familia ya Mungu. Baba yetu wa Kiroho ni Mungu peke yake tulipofanyika kuwa wana wa Mungu baada ya kumpokea Yesu kama Bwana na mwokozi wa maisha yetu, tulifanyika wana wa Mungu kwa uwezo wa Roho Mtakatifu kwa hiyo kuzaliwa kwetu kwa upya ni matokeo ya kazi ya Roho Mtakatifu na wala sio ya mwanadamu yeyote yule.

Tangu kuokolewa kwetu sisi sote tumekuwa wanafunzi wa Yesu na kila siku tunajifunza, Mwalimu wetu mkuu ni Yesu Kristo na Roho Mtakatifu kwa hiyo sisi sio Rabbis, wala mafundisho yetu asili yake sio sisi bali ni Yesu Kristo mwenyewe na Roho Mtakatifu. Kumbuka neno lile naye alitoa wengine hii maana yake yeye ndiye asili ya watumishi

Waefeso 4:11-13 “Naye alitoa wengine kuwa mitume, na wengine kuwa manabii; na wengine kuwa wainjilisti na wengine kuwa wachungaji na waalimu; kwa kusudi la kuwakamilisha watakatifu, hata kazi ya huduma itendeke, hata mwili wa Kristo ujengwe; hata na sisi sote tutakapoufikia umoja wa imani na kumfahamu sana Mwana wa Mungu, hata kuwa mtu mkamilifu, hata kufika kwenye cheo cha kimo cha utimilifu wa Kristo;”

Kristo Yesu ndiye anayetoa huduma ya kitume, kinabii, kiinjilisti, kichungaji na kialimu, wote hawa wanaongozwa na Roho Mtakatifu chanzo cha mafundisho yao ni Kristo mwenyewe na Roho Mtakatifu, kila aina ya mafundisho ya neno la Mungu asili yake ni Roho Mtakatifu yeye ndiye asili ya mafundisho yetu, Yesu alisema atakapokuja Roho wa Kweli atatufundisha na kwa sababu hiyo katika kanisa Roho wa Mungu amekuwa akitumia watu kufundisha kweli zake na kuyafunua maandiko.

Yohana 14:26 “Lakini huyo Msaidizi, huyo Roho Mtakatifu, ambaye Baba atampeleka kwa jina langu, atawafundisha yote, na kuwakumbusha yote niliyowaambia.” 

Kristo anatufundisha kuwa badala ya kutafuta heshima miongoni mwa wanadamu sisi tunapaswa kuwa watumishi wa watu, unyenyekevu ni sehemu muhimu sana inayoweza kumfanya Mungu Roho Mtakatifu kuendelea kuleta mafundisho kwetu na kutufunulia jumbe zake kwaajili ya mwili wa Kristo, sisi au mimi na wewe sio chanzo cha mafundisho hayo bali Yesu mwenyewe, Mafarisayo na waandishi walijiweka katika nafasi ya kujifikiri kuwa wao ndo chanzo cha mafundisho na kuwa mafunuo ya kweli yanatoka kwao na wao ndio wenye mamlaka ya kuamuru mtu afundishe, wasipo kuidhinisha watahakikisha haukubaliki, hivyo wakakutana na fundisho hili zito kutoka kwa Yesu Kristo. Ni kwa nini hasa Yesu alitoa fundisho hili ambalo ni kama siku za karibuni kanisa linajisahau na kuanza tena kuwaita viongozi wa kiroho baba? Mimi niiteni Mchungaji tu inanitosha kwa nini Yesu alikataza? Hapa ziko sababu:-

Kumpa Mungu heshima anayoistahili – Yesu alikuwa anataka kukazia ukweli kwamba Baba wa mbinguni ndiye baba wa kweli wa watu wote waliomuamini Bwana Yesu na kumpokea kama Bwana na mwokozi wao, Hakuna mtu mwingine anayeweza kuichukua nafasi hiyo au hata kujipa nafasi hii, Yaani ya kumuita mtu mwingine baba katika maswala ya kiroho, Heshima ya baba wa kiroho ni heshima ya Mungu baba peke yake, ikiwa mtumishi wa Mungu awaye yote atajiita baba au watu wanamuita baba anajiweka katika hatari ya kuichukua heshima ya Mungu baba au utukufu wake, kwa hiyo ni lazima tuwaelimishe watu wasituite mtu baba. 


Malaki 1:6 “Mwana humheshimu baba yake, na mtumishi humcha bwana wake; basi, kama mimi ni baba yenu, heshima yangu iko wapi? Na kama mimi ni bwana wenu, kicho changu ki wapi? Bwana wa majeshi awauliza ninyi, enyi makuhani, mnaolidharau jina langu. Nanyi mwasema, Tumelidharau jina lako kwa jinsi gani? ” 


Isaya 42:6-8 “Mimi, Bwana, nimekuita katika haki, nami nitakushika mkono, na kukulinda, na kukutoa uwe agano la watu, na nuru ya mataifa; kuyafunua macho ya vipofu, kuwatoa gerezani waliofungwa, kuwatoa wale walioketi gizani katika nyumba ya kufungwa. Mimi ni Bwana; ndilo jina langu; na utukufu wangu sitampa mwingine, wala sitawapa sanamu sifa zangu.”


Yesu anatoa tahadhari kwa kusisitiza kwamba baba wa mbinguni ndiye baba wa kweli na halisi wa watu waliookolewa au walioamini, na kwamba hakuna mtu mwingine anayeweza kuichukua nafasi hiyo, kwa hiyo unapomuita mtu mwingine baba katika maana ya heshima ya kiroho, maana yake unampa mtu heshima ambayo inamstahili Mungu pekee, Mwenyewe ana hoji kama mimi ni Baba yenu heshima yangu iko wapi? 


Kuzuia mamlaka makubwa juu ya watu – Kwaasili Mungu alipomuumba mwanadamu alikusudia wanadamu kutawala viumbe vyote, lakini sio watu kuwatawala watu, Waandishi na mafarisayo walikuwa wamejenga mfumo wa kidini ambao ulikuwa unawapa mwanya wa wao kuwa na mamlaka kubwa juu ya maisha ya watu ni wao ndio walikuwa wanaamua hata nani aishi na nani auawe, inapofikia hatua ya mwanadamu kujipa mamlaka mpaka ya kuamua ni nani atakula au nani atakaa na njaa, nani atamuoa nani, na nani ataolewa na nani?  Mungu huwa anachukizwa na hali hiyo, Mwanadamu sio mtawala wa mwanadamu mwenzake lakini ni msimamizi tu, na ndio maana mitume hawakuwahi kutengeneza mifumo ya kiutawala bali mifumo ya kimaongozi, hakuna aliyekuwa mkubwa miongoni mwa wanafunzi Yesu., Mungu ni Mungu wa utaratibu na mifumo ya kisimamizi haina shida kwake lakini kumbuka hata wazee waliochaguliwa kumsaidia Musa katika uongozi, hawajawahi kuitwa baba, wala mitume hawajawahi popote pale kujiita baba na walipotumia neno baba au mwanangu au watoto wangu wadogo, hawakutumia maneno hayo katika mtazamo wa ubora bali katika mtazamo wa uhusiano.Musa ni nabii mkubwa sana aliyekuwa na uhusiano mkubwa na wa karibu na Mungu lakini hatuoni kokote katika maandiko akiitwa baba. Badala yake yeye alimuita Mungu baba.


Mwanzo 1:28-31 “Mungu akawabarikia, Mungu akawaambia, Zaeni, mkaongezeke, mkaijaze nchi, na kuitiisha; mkatawale samaki wa baharini, na ndege wa angani, na kila kiumbe chenye uhai kiendacho juu ya nchi. Mungu akasema, Tazama, nimewapa kila mche utoao mbegu, ulio juu ya uso wa nchi yote pia, na kila mti, ambao matunda yake yana mbegu; vitakuwa ndivyo chakula chenu; na chakula cha kila mnyama wa nchi, na cha kila ndege wa angani, na cha kila kitu kitambaacho juu ya nchi, chenye uhai; majani yote ya miche, ndiyo chakula chenu; ikawa hivyo. Mungu akaona kila kitu alichokifanya, na tazama, ni chema sana. Ikawa jioni ikawa asubuhi, siku ya sita.”


Kumbukumbu 32:6 “Je! Mnamlipa Bwana hivi, Enyi watu wapumbavu na ujinga? Je! Yeye siye baba yako aliyekununua? Amekufanya, na kukuweka imara.”


Matendo 12:20-23 “Naye Herode alikuwa amewakasirikia sana watu wa Tiro na Sidoni; wakamwendea kwa nia moja, na wakiisha kufanya urafiki na Blasto, mwenye kukitunza chumba cha mfalme cha kulalia, wakataka amani; kwa maana nchi yao ilipata riziki kwa nchi ya mfalme. Basi siku moja iliyoazimiwa, Herode akajivika mavazi ya kifalme, akaketi katika kiti cha enzi, akatoa hotuba mbele yao. Watu wakapiga kelele, wakisema, Ni sauti ya Mungu, si sauti ya mwanadamu. Mara malaika wa Bwana akampiga, kwa sababu hakumpa Mungu utukufu; akaliwa na chango, akatokwa na roho.”


Herode alifikia hatua ya kuamua mtu wa kufa na mtu wa kuachiwa huru, alifikia hatua ya kuamua nani akae na njaa na nani anufaike na Mungu alimsubiria hapo baada ya kuwafunga mitume na kumuua Yakobo na kutaka kumuua Petro na kutawala watu wa Tiro na Sidoni kwa kuamua kuwanyima chakula maana wanaishi kwa mkono wake, Mungu alichukizwa na hatua hii, wakristo lazima tufikie ngazi ya kujihadhari sana kuwa na mamlaka juu ya watu, sisi ni viongozi tu wa kiroho, ni wasimamizi tu, hatuna mamlaka juu ya maisha ya watu, Mungu ametuweka kama watumishi ili tuwahudumie watu wa Mungu, na hili halimaanishi watu wa Mungu waache kuwaheshimu viongozi wa kiroho, hapana lakini sisi hatupaswi kutukuzwa, wala kujitukuza.


Kujifunza njia ya unyenyekevu – Katika tukio hili pia Bwana Yesu alikuwa akifundisha kuhusu umuhimu wa unyenyekevu, kuwakataza wanafunzi wake kuitwa baba au rabi au kiongozi alikuwa akiwaelekeza kinyume na mafarisayo na masadukayo na waandishi ya kuwa katika njia ya ufalme wa Mungu hakuna nafasi yoyote ya kujivuna na kujiona au kufikiri ya kuwa tuko juu kuliko wengine, Mungu kumuita mtu katika huduma ya  kitume, kinabii, kiinjilisti, kichungaji, na ualimu aliweka ndani mwetu huduma, na nyakati za leo uko utaratibu mzuri wa kimaongozi katika kanisa kama mtu ni Askofu mkuu ita tu Askofu mkuu, kama ni askofu wa jimbo ita tu askofu wa jimbo, kama ni mwangalizi ita tu mwangalizi, kama ni mchungaji ita tu mchungaji, ni mtume ita tu mtume, ni nabii ita tu nabii, na mwinjilisti ita tu mwinjilisti na mchungaji ita tu mchungaji, ni Mwalimu ita tu Mwalimu, ni padre ita tu padre, ni kuhani itatu tu kuhani, ni paroko ita tu paroko usimuite mtu baba, Hakuna  mahali popote katika maandiko ya agano jipya ambapo wakristo walimuita mtu baba, huduma hizo zenyewe ni heshima tosha maana zimetoka kwa Mungu, usianze na baba askofu, baba mchungaji, baba paroko, unaanza kujiingiza katika anga lingine wakati dhambi iliyomuangusha shetani ikiwa ni kiburi, sifa zilizomuinua Yesu Kristo na kumfanya awe na jina kuu kuliko yote ilikuwa ni tabia ya unyenyekevu. 


Ezekiel 28:11-17 “Ulikuwa ndani ya Adeni, bustani ya Mungu; kila jiwe la thamani lilikuwa kifuniko chako, akiki, na yakuti manjano, na almasi, na zabarajadi, na shohamu, na yaspi, na yakuti samawi, na zumaridi, na baharamani, na dhahabu; kazi ya matari yako na filimbi zako ilikuwa ndani yako; katika siku ya kuumbwa kwako zilitengenezwa tayari. Wewe ulikuwa kerubi mwenye kutiwa mafuta afunikaye; nami nalikuweka hata ukawa juu ya mlima mtakatifu wa Mungu, umetembea huko na huko kati ya mawe ya moto. Ulikuwa mkamilifu katika njia zako tangu siku ile ulipoumbwa, hata uovu ulipoonekana ndani yako. Kwa wingi wa uchuuzi wako watu walikujaza udhalimu ndani yako, nawe umetenda dhambi; kwa sababu hiyo nimekutoa kwa nguvu katika mlima wa Mungu, kama kitu kilicho najisi; nami nimekuangamiza, Ewe kerubi ufunikaye, utoke katika mawe hayo ya moto. Moyo wako uliinuka kwa sababu ya uzuri wako; umeiharibu hekima yako kwa sababu ya mwangaza wako; nimekutupa chini, nimekulaza mbele ya wafalme, wapate kukutazama.”


Wafilipi 2:5-11“Iweni na nia iyo hiyo ndani yenu ambayo ilikuwamo pia ndani ya Kristo Yesu; ambaye yeye mwanzo alikuwa yuna namna ya Mungu, naye hakuona kule kuwa sawa na Mungu kuwa ni kitu cha kushikamana nacho; bali alijifanya kuwa hana utukufu, akatwaa namna ya mtumwa, akawa ana mfano wa wanadamu; tena, alipoonekana ana umbo kama mwanadamu, alijinyenyekeza akawa mtii hata mauti, naam, mauti ya msalaba. Kwa hiyo tena Mungu alimwadhimisha mno, akamkirimia Jina lile lipitalo kila jina; ili kwa jina la Yesu kila goti lipigwe, la vitu vya mbinguni, na vya duniani, na vya chini ya nchi; na kila ulimi ukiri ya kuwa YESU KRISTO NI BWANA, kwa utukufu wa Mungu Baba.”


Yesu hakumaanisha kuwa tusiwaite baba zetu wa kutuzaa kuwa baba, maandiko yanaposema tuwahehimu wazazi moja wapo ya sehemu ya heshima hiyo ni kuwaita kwa majina yao mzazi wa kiume baba na mzazi wa kike mama na tunapaswa kuwaheshimu. Wala Yesu hajafundisha kuwa tuache kuwaheshimu viongozi wetu wa kidini na kiimani na wa kiserikali tunapaswa kuwaheshimu sawasawa na madaraka ambayo Mungu amewapa na kuwanyenyekea 


1Timotheo 5:17 “Wazee watawalao vema na wahesabiwe kustahili heshima maradufu; hasa wao wajitaabishao kwa kuhutubu na kufundisha.”


Neno watawalao katika lugha ya kiyunani linalotumika hapo ni “Proistēmi” maana yake kwa kiingereza ni to preside – to be in a position of authority in a meeting or gathering, na neno lingine ni rule – governing au conducting a procedure, kwa Kiswahili kutawala kunakotajwa hapo ni mtu mwenye mamlaka ya kuongoza mkutano au kanisa, au kuendesha utaratibu, kwa msingi huo maandiko hayazungumzii kudhibiti “control” na watumishi wa Mungu wameonywa kuacha tabia ya kujifanya mabwana (Boss) katika mitaa yao


1Petro 5:1-3 “Nawasihi wazee walio kwenu, mimi niliye mzee, mwenzi wao, na shahidi wa mateso ya Kristo, na mshirika wa utukufu utakaofunuliwa baadaye; lichungeni kundi la Mungu lililo kwenu, na kulisimamia, si kwa kulazimishwa, bali kwa hiari kama Mungu atakavyo; si kwa kutaka fedha ya aibu, bali kwa moyo. WALA SI KAMA WAJIFANYAO MABWANA JUU YA MITAA YAO, bali kwa kujifanya vielelezo kwa lile kundi. 


Petro anaeleza Mungu anavyotaka watu waongozwe si kama tujifanyao mabwana juu ya mitaa bali vielelezo kwa kundi, neno hilo mabwana maana yake “Boss” ambao lina tafasiri mbaya sana, na tunapoitwa baba ni kama tunaelekea huko, uongozi wa kikristo unatupa tahadhari sana kujilinda na kujihami kiasi cha kutokuangukia katika lawama na mtego wa ibilisi, mtego wa ibilisi ni kiburi na majivuno na hukumu ya ibilisi ni anguko linalotokana na kiburi na majivuno au kujiinua na hivyo kutupiliwa mbali nje ya neema ya Mungu


1Timotheo 3:6-7 “Wala asiwe mtu aliyeongoka karibu, asije akajivuna akaanguka katika hukumu ya Ibilisi. Tena imempasa kushuhudiwa mema na watu walio nje; ili asianguke katika lawama na mtego wa Ibilisi.”


Njia iliyo bora wakati wote ni kujifunza unyenyekevu kutoka moyoni na kuwa na tahadhari, shetani anaweza kuwatumia washirika wetu kutuingiza katika mtego wa ibilisi kwani wakati mwingine ni wao ndio wanaotuita baba hivyo hatuna budi kulikataa hilo na kuwafundisha kwamba ukiniita tu Mchungaji hiyo imetosha ni heshima kubwa na kuwa kuniita baba ni kunipalia makaa, tunaye baba mmoja baba wa roho zetu, Mungu.


Kujilinda na kujiweka katika nafasi ya Mungu – Mafarisayo na waandishi walijikweza mno kiasi cha kujiweka katika ngazi ya kutumikiwa na sio kuwatumikia watu, kujiinua sana kungewaweka katika hatari ya kujiweka katika nafasi ya Mungu, Bwana Yesu alikuwa anataka kututahadharisa na hilo, aidha Yesu alikuwa akionyesha tofauti ya mafundisho yake na yale ya ulimwengu huu, watu wa ulimwengu huu wanatafuta kujikweza na mwisho wa siku watahukumiwa na kutupwa chini, lakini wale wanaotubu na kunyenyekea watainuliwa 


Mathayo 18:1-4 “Saa ile wanafunzi wakamwendea Yesu wakisema, Ni nani basi aliye mkuu katika ufalme wa mbinguni? Akaita mtoto mmoja, akamweka katikati yao, akasema, Amin, nawaambia, Msipoongoka na kuwa kama vitoto, hamtaingia kamwe katika ufalme wa mbinguni. Basi, ye yote ajinyenyekeshaye mwenyewe kama mtoto huyu, huyo ndiye aliye mkuu katika ufalme wa mbinguni.”


Marko 9:35 “Akaketi chini, akawaita wale Thenashara akawaambia, Mtu atakaye kuwa wa kwanza atakuwa wa mwisho kuliko wote, na mtumishi wa wote.


1Petro 5:5-6 “Vivyo hivyo ninyi vijana, watiini wazee. Naam, ninyi nyote jifungeni unyenyekevu, mpate kuhudumiana; kwa sababu Mungu huwapinga wenye kiburi, lakini huwapa wanyenyekevu neema.Basi nyenyekeeni chini ya mkono wa Mungu ulio hodari, ili awakweze kwa wakati wake;” 

Neno la Mungu linawataka wanafunzi wote wa Yesu kujivika unyenyekevu, na unyenyekevu wa kweli sio maigizo ni unyenyekevu kutoka ndani, kila mtu ajione na kujifunza kuwa hastahili mbele za Mungu na kuwa mtumwa wa wengine, mtu mnyenyekevu anatambua ya kuwa anayafanya yote kwa neema ya Mungu, unyenyekevu sio tabia rahisi kama tunavyodhani sababu kubwa ni kuwa kinyume cha unyenyekevu ni majivuno na kiburi jambo ambalo ndio dhambi ya ndani zaidi ya mwanadamu, ambayo shetani aliwaingizia wanadamu. 


Mwanzo 3:4-5 “Nyoka akamwambia mwanamke, Hakika hamtakufa, kwa maana Mungu anajua ya kwamba siku mtakayokula matunda ya mti huo, mtafumbuliwa macho, nanyi MTAKUWA KAMA MUNGU, mkijua mema na mabaya.” 


Shetani alitamani kuwa kama Mungu na ni aina hii ya wazo aliingiza kwa wanadamu na wakamkosea Mungu, kwa msingi huo ni lazima tuchukue tahadhari kuwa neno lolote, cheo chochote na nafasi yoyote ile ambayo anayestahili ni Mungu sisi ni lazima tujifunze kuwa mbali nayo, na sasa kwa bahati isiyo njema katazo hili la wanadamu kuitwa baba limetolewa na Yesu mwenyewe, je unataka kuabudiwa? Jilinde tujilinde na namna yoyote ile ya kutaka kuchukua nafasi ya Mungu, Yesu alihakikisha wakati wote nafasi ya ubaba inakwenda kwa anayestahili na ukichunguza katika maandiko Yesu ndiye anayeongoza kwa kutumia neno baba kuliko mtu awaye yote, Yesu amemtaja Mungu kwa kutumia neno baba mara zaidi ya 165 katika injili pekee mkazo huu sio wa kijinga, wala wa kupuuziwa wakati katika maandiko mengine ya kiyahudi ikiwepo agano la kale watu wamemtaja Mungu kama baba mara 15 tu, hii sio kwa sababu tu Yesu alikuwa mwana wa Mungu, bali kwa sababu Yesu alitaka uhusiano wa wanafunzi wake kwa Mungu uwe hivyo na kuwa mwenye sifa ya kuitwa baba ni Mungu peke yake.


Mathayo 23:8-12 “Bali ninyi msiitwe Rabi, maana mwalimu wenu ni mmoja, nanyi nyote ni ndugu.Wala msimwite mtu baba duniani; maana Baba yenu ni mmoja, aliye wa mbinguni. Wala msiitwe viongozi; maana kiongozi wenu ni mmoja, naye ndiye Kristo. Naye aliye mkubwa wenu atakuwa mtumishi wenu.Na ye yote atakayejikweza, atadhiliwa; na ye yote atakayejidhili, atakwezwa


Yohana 14:6-11 “Yesu akamwambia, Mimi ndimi njia, na kweli, na uzima; mtu haji kwa Baba, ila kwa njia ya mimi. Kama mngalinijua mimi, mngalimjua na Baba; tangu sasa mnamjua, tena mmemwona. Filipo akamwambia, Bwana, utuonyeshe Baba, yatutosha.Yesu akamwambia, Mimi nimekuwapo pamoja nanyi siku hizi zote, wewe usinijue, Filipo? Aliyeniona mimi amemwona Baba; basi wewe wasemaje, Utuonyeshe Baba? Husadiki ya kwamba mimi ni ndani ya Baba, na Baba yu ndani yangu? Hayo maneno niwaambiayo mimi siyasemi kwa shauri langu; lakini Baba akaaye ndani yangu huzifanya kazi zake. Mnisadiki ya kwamba mimi ni ndani ya Baba, na Baba yu ndani yangu; la! Hamsadiki hivyo, sadikini kwa sababu ya kazi zenyewe.”


Wakati wote Yesu alihakikisha anamtambua baba yake na alimuita baba katika maeneo mengi sana, leo hii ukitaja baba basi lazima ufafanue ni yupi anazungumzwa, yaani yuko mwanadamu fulani tu mwenye madhaifu kibao anajiita baba, Mungu na atusaidie, ikiwa watu wanatuita hivyo tunaweza kuwafundisha na tunaweza kuwakataza na kuwafunulia maandiko ili wasituingize mtegoni, nao pia wasiingie mtegoni.


Matendo 14:8-15 “Na huko Listra palikuwa na mtu mmoja, dhaifu wa miguu, kiwete tangu tumboni mwa mamaye, ambaye hajaenda kabisa. Mtu huyo alimsikia Paulo alipokuwa akinena; ambaye akamkazia macho na kuona ya kuwa ana imani ya kuponywa, akasema kwa sauti kuu, Simama kwa miguu yako sawasawa. Akasimama upesi akaenda. Na makutano walipoona aliyoyafanya Paulo wakapaza sauti zao, wakisema kwa Kilikaonia, Miungu wametushukia kwa mifano ya wanadamu. Wakamwita Barnaba, Zeu, na Paulo, Herme, kwa sababu ndiye aliyekuwa mnenaji. Kuhani wa Zeu ambaye hekalu lake lilikuwa mbele ya mji, akaleta ng'ombe na taji za maua hata malangoni, akitaka kutoa dhabihu pamoja na makutano. Walakini mitume Barnaba na Paulo, walipopata habari, wakararua nguo zao, wakaenda mbio wakaingia katika makutano, wakipiga kelele, wakisema, Akina bwana, mbona mnafanya haya? Sisi nasi tu wanadamu hali moja na ninyi; twawahubiri habari njema, ili mgeuke na kuyaacha mambo haya ya ubatili na kumwelekea Mungu aliye hai, aliyeumba mbingu na nchi na bahari na vitu vyote vilivyomo;”


Roho Mtakatifu hutuelekeza wa kumuita baba – Ni muhimu kufahamu kuwa watu wote waliompokea Yesu Kristo kama Bwana na mwokozi wa maisha yao na kuamini katika kazi aliyoifanya pale msalabani wanapewa neema ya kufanyika watoto wa Mungu, watu hawa wanazaliwa kwa mapenzi ya Mungu na sio ya mtu au mwili kwa sababu hiyo ni wana wa Mungu, kwa hiyo Mungu Roho Mtakatifu huwaelekeza watoto wake nani wa kumuita baba ona  


Yohana 1:12-13 “Bali wote waliompokea aliwapa uwezo wa kufanyika watoto wa Mungu, ndio wale waliaminio jina lake; waliozaliwa, si kwa damu, wala si kwa mapenzi ya mwili, wala si kwa mapenzi ya mtu, bali kwa Mungu.”


Sio hivyo tu Biblia inatufundisha kuwa Roho Mtakatifu huweka mzigo ndani yetu kumuita Mungu baba kwa sababu yeye ndiye aliyewazaa kiroho kwa mapenzi yake na anatujulisha kuwa Mungu ndiye baba yetu na ya kuwa uhusiano wa karibu sana tulio nao watu tuliookolewa na Mungu ni uhusiano wa baba na mwana wake


Wagalatia 4:4-7 “Hata ulipowadia utimilifu wa wakati, Mungu alimtuma Mwanawe ambaye amezaliwa na mwanamke, amezaliwa chini ya sheria, kusudi awakomboe hao waliokuwa chini ya sheria, ili sisi tupate kupokea hali ya kuwa wana. Na kwa kuwa ninyi mmekuwa wana, Mungu alimtuma Roho wa Mwanawe mioyoni mwetu, aliaye, Aba, yaani, Baba. Kama ni hivyo, wewe si mtumwa tena bali u mwana; na kama u mwana, basi, u mrithi kwa Mungu.”


Warumi 8:14-15 “Kwa kuwa wote wanaoongozwa na Roho wa Mungu, hao ndio wana wa Mungu. Kwa kuwa hamkupokea tena roho wa utumwa iletayo hofu; bali mlipokea roho ya kufanywa wana, ambayo kwa hiyo twalia, Aba, yaani, Baba.”


Warumi 8:15-16 “Roho mwenyewe hushuhudia pamoja na roho zetu, ya kuwa sisi tu watoto wa Mungu; na kama tu watoto, basi, tu warithi; warithi wa Mungu, warithio pamoja na Kristo; naam, tukiteswa pamoja naye ili tupate na kutukuzwa pamoja naye.”


Abba”  ni neno linalotumika katika kiyunani kuonyesha uhusiano wa ndani zaidi wa mtu na baba yake ni neno lililolotumiwa na watoto wadogo kuita baba zao waliowazaa, Roho Mtakatifu tunapookoka anaweka hiyo hali ndani yetu tuliookolewa kuelekeza neno baba kwa Mungu wetu aliyetuumba na kutuokoa, kuonyesha uhusiano wa ndani tulio nae kama watoto wake, sasa basi ikiwa Roho Mtakatifu hutuelekeza sisi kumuita Mungu baba yetu, swali ni nani anayetuelekeza kumuita mtu wa kawaida ambaye ni kiongozi wa kiroho nani anatuelekeza kumuita baba? Usinijibu swali hilo! Ubaba wote wa mbinguni na duniani unaelekezwa wapi?


Waefeso 3:14-15 “Kwa hiyo nampigia Baba magoti, ambaye kwa jina lake ubaba wote wa mbinguni na wa duniani unaitwa,”


Kristo alikazia sana kutuelekeza kwa baba – Kama ilivyo kwa Roho wa Mungu kutufundisha na kutuelekeza wa kumuita baba, ni ukweli ulio wazi kuwa katika maandiko Yesu Kristo katika maisha na mafundisho yake alikazia sana sana sana neno baba akilielekeza kwa Mungu baba, kulikuwa na sababu maalumu sana za Yesu kulikazia hili, na ziko sababu maalumu za Roho Mtakatifu kutufundisha kumuita Mungu kama baba yetu, Kama Yesu ni kiongozi mkuu wa wokovu wetu na kama kweli tunafuata nyayo zake utaweza kuona akikazia katika maeneo mbalimbali katika maandiko akikazia kuhusu ubaba wa Mungu wetu.


Mathayo 11:25-27 “Wakati ule Yesu akajibu, akasema, Nakushukuru, Baba, Bwana wa mbingu na nchi, kwa kuwa mambo haya uliwaficha wenye hekima na akili, ukawafunulia watoto wachanga. Naam, Baba, kwa kuwa ndivyo ilivyopendeza mbele zako. Akasema, Nimekabidhiwa vyote na baba yangu; wala hakuna amjuaye Mwana, ila Baba; wala hakuna amjuaye Baba, ila Mwana, na ye yote ambaye Mwana apenda kumfunulia.”


Marko 14:35-36 “Akaendelea mbele kidogo, akaanguka kifudifudi, akiomba ya kuwa, ikiwezekana, saa hiyo imwepuke.Akasema, Aba, Baba, yote yawezekana kwako; uniondolee kikombe hiki; walakini, si kama nitakavyo mimi, bali utakavyo wewe.”


Luka 23:34 “Yesu akasema, Baba, uwasamehe, kwa kuwa hawajui watendalo. Wakagawa mavazi yake, wakipiga kura.”


Yohana 14:6-10 “Yesu akamwambia, Mimi ndimi njia, na kweli, na uzima; mtu haji kwa Baba, ila kwa njia ya mimi. Kama mngalinijua mimi, mngalimjua na Baba; tangu sasa mnamjua, tena mmemwona. Filipo akamwambia, Bwana, utuonyeshe Baba, yatutosha. Yesu akamwambia, Mimi nimekuwapo pamoja nanyi siku hizi zote, wewe usinijue, Filipo? Aliyeniona mimi amemwona Baba; basi wewe wasemaje, Utuonyeshe Baba? Husadiki ya kwamba mimi ni ndani ya Baba, na Baba yu ndani yangu? Hayo maneno niwaambiayo mimi siyasemi kwa shauri langu; lakini Baba akaaye ndani yangu huzifanya kazi zake.”


Yohana 17:1-5 “Maneno hayo aliyasema Yesu; akainua macho yake kuelekea mbinguni, akasema, Baba, saa imekwisha kufika. Mtukuze Mwanao, ili Mwana wako naye akutukuze wewe; kama vile ulivyompa mamlaka juu ya wote wenye mwili, ili kwamba wote uliompa awape uzima wa milele.Na uzima wa milele ndio huu, Wakujue wewe, Mungu wa pekee wa kweli, na Yesu Kristo uliyemtuma. Mimi nimekutukuza duniani, hali nimeimaliza kazi ile uliyonipa niifanye. Na sasa, Baba, unitukuze mimi pamoja nawe, kwa utukufu ule niliokuwa nao pamoja nawe kabla ya ulimwengu kuwako.”


Yohana 17:21-26 “Wote wawe na umoja; kama wewe, Baba, ulivyo ndani yangu, nami ndani yako; hao nao wawe ndani yetu; ili ulimwengu upate kusadiki ya kwamba wewe ndiwe uliyenituma. Nami utukufu ule ulionipa nimewapa wao; ili wawe na umoja kama sisi tulivyo umoja. Mimi ndani yao, nawe ndani yangu, ili wawe wamekamilika katika umoja; ili ulimwengu ujue ya kuwa ndiwe uliyenituma, ukawapenda wao kama ulivyonipenda mimi.Baba, hao ulionipa nataka wawe pamoja nami po pote nilipo, wapate na kuutazama utukufu wangu ulionipa; kwa maana ulinipenda kabla ya kuwekwa msingi ulimwengu. Baba mwenye haki, ulimwengu haukukujua; lakini mimi nalikujua, na hao wamejua ya kuwa ndiwe uliyenituma. Nami naliwajulisha jina lako, tena nitawajulisha hilo; ili pendo lile ulilonipenda mimi liwe ndani yao, nami niwe ndani yao.”


Mitume walielekeza watu kwa baba – Unapoangalia katika nyaraka zote za maelekezo na mafundisho ya mitume utaweza kuona wakilitii agizo la Yesu Kristo kwa kumtaja Mungu kama Baba, kwa hiyo ni wazi kuwa mamlaka ya ubaba ilipelekwa kwa usahihi kwa Mungu baba mwenyewe na wala sio kwa wanadamu, Wazo la ubaba wa Mungu halikuwa na Msingi sana katika agano la kale , lakini limekuwa ni jambo la msingi sana katika nyakati za gano jipya, huku Yesu akilitilia mkazo sana kuonyesha ni mapenzi ya Mungu, Baba aitwe baba, kwa hiyo utaweza kuona mitume waliukazia ubaba huu kuliko tunavyofikiri kumbuka kuwa mitume walikuwa makini sana, Yesu alifanya hivyo ili sisi tushike hili na kulitumia, labda limesahaulika lakini huu ndio wakati sahihi sasa wa kulikumbusha kanisa msituite baba, tunaye baba mmoja tu ndiye Mungu muumba.


1Wakorintho 8:6 “lakini kwetu sisi Mungu ni mmoja tu, aliye Baba, ambaye vitu vyote vimetoka kwake, nasi tunaishi kwake; yuko na Bwana mmoja Yesu Kristo, ambaye kwake vitu vyote vimekuwapo, na sisi kwa yeye huyo.”


1Wakorintho 1:3 “Neema na iwe kwenu na amani, zitokazo kwa Mungu Baba yetu, na kwa Bwana Yesu Kristo.”


Wagalatia 4:6 “Na kwa kuwa ninyi mmekuwa wana, Mungu alimtuma Roho wa Mwanawe mioyoni mwetu, aliaye, Aba, yaani, Baba.”


Warumi 1:7 “kwa wote walioko Rumi, wapendwao na Mungu, walioitwa kuwa watakatifu. Neema na iwe kwenu na amani itokayo kwa Mungu Baba yetu, na kwa Bwana Yesu Kristo.”


Waefeso 5:19-21 “mkisemezana kwa zaburi na tenzi na nyimbo za rohoni, huku mkiimba na kumshangilia Bwana mioyoni mwenu; na kumshukuru Mungu Baba sikuzote kwa mambo yote, katika jina lake Bwana wetu Yesu Kristo; hali mnanyenyekeana katika kicho cha Kristo.”


Wakolosai 1:2 “kwa ndugu watakatifu, waaminifu katika Kristo, walioko Kolosai. Neema na iwe kwenu, na amani, zitokazo kwa Mungu Baba yetu.”


2Yohana 1:9 “Kila apitaye cheo, wala asidumu katika mafundisho ya Kristo, yeye hana Mungu. Yeye adumuye katika mafundisho hayo, huyo ana Baba na Mwana pia.”


1Yohana 2:1 “Watoto wangu wadogo, nawaandikia haya ili kwamba msitende dhambi. Na kama mtu akitenda dhambi tunaye Mwombezi kwa Baba, Yesu Kristo mwenye haki,“


1Yohana 4:14 “Na sisi tumeona na kushuhudia ya kuwa Baba amemtuma Mwana kuwa Mwokozi wa ulimwengu.


Yakobo 1:17 “Kila kutoa kuliko kwema, na kila kitolewacho kilicho kamili, hutoka juu, hushuka kwa Baba wa mianga; kwake hakuna kubadilika, wala kivuli cha kugeuka-geuka.”


1Wathesalonike 1:1-2 “Paulo, na Silwano, na Timotheo, kwa kanisa la Wathesalonike, lililo katika Mungu Baba, na katika Bwana Yesu Kristo. Neema na iwe kwenu na amani. Twamshukuru Mungu siku zote kwa ajili yenu nyote, tukiwataja katika maombi yetu.” 


Hitimisho


Msimwite mtu baba Duniani. Ni agizo la Bwana Yesu lililo la muhimu sana, Yesu alitaka kila mkristo aelewe  kuwa uhusiano wetu na Mungu ni wa karibu zaidi, Mungu ni Baba yetu na heshima yake kubwa ni ubaba wake ambao kimsingi heshima hii haipaswi kutolewa kwa mwingine kirahisi, kwa msingi huo katika maisha yetu ya kiroho tunaye baba mmoja tu ndiye Mungu. Nanyi msalipo semeni, Baba yetu uliye mbinguni ona:-


Mathayo 6:9-12 “Basi ninyi salini hivi; Baba yetu uliye mbinguni, Jina lako litukuzwe, Ufalme wako uje, Mapenzi yako yatimizwe, hapa duniani kama huko mbinguni.Utupe leo riziki yetu.Utusamehe deni zetu, kama sisi nasi tuwasamehevyo wadeni wetu. Na usitutie majaribuni, lakini utuokoe na yule mwovu. [Kwa kuwa ufalme ni wako, na nguvu, na utukufu, hata milele. Amina.]


Yesu alitaka watu wote waelewe kuwa Mungu pekee ndiye baba naye alikuja kutupa kielelezo tukifuate wengine wote wanaobaki ni watumishi wa Mungu kwaajili ya maisha yetu ya kiroho, ni wasimamizi tu, hawana mamlaka ya kutawala wanadamu, wana mamlaka ya kusimamia, heshima ya u baba ni ya Mungu pekee, Waandishi na mafarisayo walikuwa wamejenga mfumo ambao kwa bahati mbaya sana miaka ya hivi karibuni unarudi kwa kasi, mifumo inayowaruhusu wao kuwa na mamlaka makubwa juu ya watu, Yesu alitaka watu wasiwategemee viongozi wa kidini, Yesu alikataa mfumo huo na kuwakumbusha watu kuwa wanapaswa kumtegemea Mungu pekee. Aidha Yesu alitaka watu wawe wanyenyekevu na kuacha kujipa majina makubwa kwani kwa makusudi ya kupata heshima, uhusiano wetu na viongozi wa kidini na wao ni watu hauwezi kuwa uhusiano wa karibu kama uhusiano wetu na Mungu Baba, Hivyo ni Mungu pekee ndiye baba yetu, najua kuna watu wanaweza kuchukizwa na fundisho hili, lakini ni ukweli ulio wazi hatuwezi kuwa na akili au hekima kumzidi Yesu Kristo, kama Yesu amekataza wewe una nini? Endelea kujiita baba lakini yatakayokukuta mie simo, kazi yangu ni kukufunulia kweli za neno la Mungu na ni juu yako kuelewa, kutii au kuasi kukubali au kubisha. Lakini ukweli uko wazi kuwa washirika wengi sana nyakati za leo wanatuita baba, kila mahali ninakoenda nikijitambulisha kama mchungaji watu wanaita baba, ukweli sijawahi kuwakataza lakini moyoni ninapata taabu sana kwanini wakristo wanaacha kuniita mchungaji wananiita baba? Au kwa nini waniite baba mchungaji wakati nadhani ukiniita mchungaji tu inatosha, Ni ukweli ulio wazi kuwa mimi najua kuwa hawakuwa wamejifunza neno na agizo la Yesu na kulifikiri kwa kina lakini ilivyo ni kwamba hata Yesu hatumuiti baba, iweje Yesu aje akute mimi naitwa baba jina ambalo yeye hajawahi kulitumia wala Roho Mtakatifu hajawahi kutuongoza tumuite Yesu baba, wala mitume hawajafundisha wakristo kumuita mtu baba, wala biblia haijaelekeza kumuita mtu baba, alafu hapa kuna mtu mwanadamu tunamuita baba? Yesu Kristo mpaka dakika ya mwisho akiwa anapaa bado alikuwa akimtaja Mungu baba kama baba ona hii


Matendo 1:4-8 “Hata alipokuwa amekutana nao aliwaagiza wasitoke Yerusalemu, bali waingoje ahadi ya Baba, ambayo mlisikia habari zake kwangu; ya kwamba Yohana alibatiza kwa maji, bali ninyi mtabatizwa katika Roho Mtakatifu baada ya siku hizi chache. Basi walipokutanika, wakamwuliza, wakisema, Je! Bwana, wakati huu ndipo unapowarudishia Israeli ufalme? Akawaambia, Si kazi yenu kujua nyakati wala majira, Baba aliyoyaweka katika mamlaka yake mwenyewe. Lakini mtapokea nguvu, akiisha kuwajilia juu yenu Roho Mtakatifu; nanyi mtakuwa mashahidi wangu katika Yerusalemu, na katika Uyahudi wote, na Samaria, na hata mwisho wa nchi.”


Kwa hiyo sasa itakuwaje? Kanisa hatuna budi kutubu, na kuacha mara moja kuwaita watumishi wa Mungu wowote wale Baba, watumishi wa Mungu ni lazima tukatae kuitwa baba, na ni muhimu kuwafundisha watu wote duniani kuacha mara moja kutuita baba, hivi hujawahi kujiuliza ni kwanini Mashehe na mamufti na viongozi wakubwa wa dini kama ya kiislamu hawawaiti viongozi wao wa dini baba?  na sasa wengine tumeenda mbali sana mpaka tuna BABA MTAKATIFU. Hii ni kufuru kubwa sana narudia tena hii ni kufuru kubwa sana narudia mara ya tatu hii ni kufuru kubwa sana, Shetani kuna mahali anataka kutupeleka taratibu bila sisi kujielewa, ile ile tabia yake ya kutaka kuwa kama Mungu anaipanda kwetu na kutuingizia bila kujua mwisho majina yote ya Mungu yatakuwa ndio ya wanadamu ni lazima tuwe makini na hili ndilo Mungu alinituma niweze kuwaonya watu, angalia kwa mujibu wa Yesu Kristo BABA MTAKATIFU ni nani? Ona:- 


Yohana 17:11-12. “Wala mimi simo tena ulimwenguni, lakini hawa wamo ulimwenguni, nami naja kwako. BABA MTAKATIFU, kwa jina lako ulilonipa uwalinde hawa, ili wawe na umoja kama sisi tulivyo. Nilipokuwapo pamoja nao, mimi naliwalinda kwa jina lako ulilonipa, nikawatunza; wala hapana mmojawapo wao aliyepotea, ila yule mwana wa upotevu, ili andiko litimie.”


Makanisa yanayoongoza kwa kuita wachungaji na makuhani wao baba ni pamoja na Catholics, Orthodox, Anglican na Lutheran kwa bahati mbaya siku hizi hata watu waliookoka wameanza kuwaita wachungaji baba, Hata Haruni alikuwa ni kuhani mkuu lakini Wayahudi hawakumuita baba, kule kuchaguliwa tu na Mungu umtumikie ni heshima kubwa sana na inatosha. 


Lakini ni kwanini Catholics, Orthodox, Anglican na Lutheran huwaina makuhani wao na viongozi wao wa dini Baba? Akijibu swali hili Padre Colin Wen ambaye ni kuhani wa kikatoliki yeye alijibu hivi!


“Sio vibaya kabisa kumuita mtu mwingine baba sawa na katazo la Kristo katika Mathayo 23:9 yeye alisema kuwa mstari huu, unaweza kuwa umetafasiriwa vibaya kwa kuzingatia muktadha wa kile alichokuwa anakisema Bwana Yesu, Yesu hapa alikuwa anakemea tabia ya waandishi namafarisayo ambao waliweka mkazo wa kutafuta heshima hata kuliko utumishi wao kwa Mungu, Padre Colin Wen anaendelea kueleza kuwa ni kweli tuna baba mmoja tu wa mbinguni lakini makuhani wa kidini na wengine wanaoitwa baba wanatumia jina hili kwa sababu wanahusika katika ubaba huo kupitia utumishi wao,  na hivyo sio vibaya wakiitwa baba, wao sio baba kimamlaka lakini wanamuwakilisha baba mbinguni, kama jinsi ambavyo wao sio baba wa kimwili, aliongeza kuwa hata kuwaita baba viongozi wa kiroho maaskofu na makunani sio kitu ambacho kimeibuka siku za karibuni  kwani hata Paulo mwenyewe anasema 


1Wakorintho 4:14-15 “Siyaandiki hayo ili kuwatahayarisha; bali kuwaonya kama watoto niwapendao. Kwa kuwa ijapokuwa mna waalimu kumi elfu katika Kristo, walakini hamna baba wengi. Maana mimi ndimi niliyewazaa katika Kristo Yesu kwa njia ya Injili.”


Kwa maelezo hayo anasema Paulo alijiona kuwa anafiti kabisa kujiita baba na akaeleza kuwa katika maandiko Petro, Paulo na Yohana wote waliwaona waamini wao kama watoto katika mtazamo wa kuwaona wao kuwa ni familia yao na kuwa uhusiano waliokuwa nao ulikuwa ni kama uhusiano wa baba na mwana anasema Petro alimuita Marko mwanangu , na Yohana akiwaita wakristo wanae


1Petro 5:12-13 “Kwa mkono wa Silwano, ndugu mwaminifu kama nionavyo, nimewaandikia kwa maneno machache, kuonya na kushuhudia ya kuwa hii ndiyo neema ya kweli ya Mungu. Simameni imara katika hiyo. Mwenzenu mteule hapa Babeli awasalimu, na Marko mwanangu.”


1Yohana 2:1-2 “Watoto wangu wadogo, nawaandikia haya ili kwamba msitende dhambi. Na kama mtu akitenda dhambi tunaye Mwombezi kwa Baba, Yesu Kristo mwenye haki, naye ndiye kipatanisho kwa dhambi zetu; wala si kwa dhambi zetu tu, bali na kwa dhambi za ulimwengu wote.” 


Anaeleza kuwa tabia hii iliendelea kuwa tabia ya kanisa kwa nyakati zote za maisha ya kanisa na akaeleza ndio maana Askofu mkuu wa kanisa Catholic anatumia jina Papa kama ilivyo kwa kiongozi wa kanisa la Coptic la huko Misri tangu enzi na enzi, Je hoja hizi zinajitosheleza? Kujenga fundisho? Kuwa watumishi wa Mungu wanaushiriki ubaba katika huduma na kwa sababu hiyo kuitwa kwao baba sio tatizo? Padre Colin Wen anaona kuwa japo wao sio baba wa kibailojia, lakini wanashiriki ubaba kila siku katika huduma kuanzia ubatizo na sakramenti nyinginezo na anaeleza kuwa kila siku katika huduma yake anashiriki ubaba huo na anauona na anasema anapoitwa baba inamkubusha kuwa yeye ni nani”. Mwisho wakumnukuu.


Kwa mtazamo wangu mimi naona Padre Colin Wen hoja zake hazina mashiko, kitendo cha kuchaguliwa tu na Mungu kuwa kuhani au Padre tayari kwa Mungu ni heshima kubwa sana, wangeridhika tu kuitwa Padre, au kuhani, au kasisi, na siew engine Mchungaji inatosha lakini nionavyo mimi kuna mstari mwembamba sana kati ya katazo la Yesu Kristo na utetezi wa kuitwa baba tunaoutaka na mtazamo mpana wa kibiblia, Petro kumuita Marko mwanangu, au Paulo kumuita Timotheo mwanangu, au Yohana kuwaita wakristo wanae, inaweza kuwa sio tatizo kwanza kwa sababu ya ukaribu mkubwa wa kimahusiano walio nao Petro na Marko na hali kadhalika Paulo na Timotheo, kama nilivyotangulia kufafanua hapo juu kwenye jinsi na namna neno baba lilivyoelezewa maana zake, lakini pia Umri wao ukilinganisha na washirika waliokuwepo wakati huo mfano Yohana alikuwa mzee sana ukilinganisha na washirika waliokuwako wakati huo kwa umri wake kutumia neno mwanangu haikuwa kitu cha kushangaza. Paulo na Timotheo walikuwa na ukaribu kiasi ambacho Timotheo alitahiriwa nadhani chini ya mamlaka ya Paulo na kama sio Paulo mwenyewe, wao walikuwa na uhusiano wa karibu na kihisia. 


Matendo 16:1-3 “Basi akafika Derbe na Listra, na hapo palikuwa na mwanafunzi mmoja jina lake Timotheo, mwana wa mwanamke Myahudi aliyeamini; lakini babaye alikuwa Myunani. Mtu huyo alishuhudiwa vema na ndugu waliokaa Listra na Ikonio. Paulo akamtaka huyo afuatane naye, akamtwaa akamtahiri kwa ajili ya Wayahudi waliokuwako pande zile; kwa maana wote walijua ya kuwa babaye ni Myunani.”


Kwa hiyo unaweza kuona uhusiano wa Paulo na Timotheo ulikuwa wa ndani kiasi ambacho Timotheo kuitwa mwanangu na Paulo halikuwa jambo la kushangaza, sina Muda sana wa kuzungumzia Marko Kwa Petro, Lakini wote tunajua jinsi ambavyo Petro alifahamiana na Marko tangu akiwa kijana mdogo katika jengo lililokuwako Yerusalem siku ya Pentekoste, na historia ya kanisa inaonyesha uhusiano huo, aidha ukubwa wa umri wa Yohana ambaye aliishi siku nyingi kuwaita wanae washirika pia sio jambo la kushangaza, na zaidi ya yote katazo la Kristo msimuite mtu baba, lilikuwa kwa wanafunzi wa Yesu tusimuite mtu baba duniani, sisi sasa ndio wanafunzi wa Yesu na swala hilo linatuhusu, lakini hatujakatazwa kumuita mtu mwanangu. Katazo linawahusu watu wasituite baba, tunaweza kujenga hoja za kimaandiko na Roho Mtakatifu Mwalimu mkuu anaweza kutufafanulia kama ni haki kuitwa baba katika uhusiano wa kiroho! Kwa sababu Baba ndiye Mwanzilishi wa Maisha yetu sifa ya Ubaba ni sifa ya Mungu peke yake na sio sisi, makasisi wa kikatoliki waitwe Padre, maksaisi wa kiprotestant na waitwe wachungaji, na majina mengineyo lakini hata hivyo swala la kuitwa baba katika uhusiano wa Kiroho linatuweka katika wakati mgumu ambao hakuna hoja ya kimaandiko ya kututetea.



Na Rev. Innocent Samuel Kamote


Mkuu wa wajenzi mwenye Hekima