Ijumaa, 19 Aprili 2019

Mwondoshe huyu, utufungulie Baraba.!


Luka 23:18-25Wakapiga kelele wote pamoja, wakisema, Mwondoe huyu, utufungulie Baraba.  Naye ni mtu aliyetupwa gerezani kwa ajili ya fitina iliyotokea mjini, na kwa uuaji Basi Pilato alisema nao mara ya pili, kwa vile alivyotaka kumfungua Yesu.  Lakini wakapiga kelele, wakisema, Msulibishe. Msulibishe. Akawaambia mara ya tatu, Kwa sababu gani? Huyu ametenda uovu gani? Sikuona kwake hata neno lipasalo kufa. Basi nikiisha kumrudi nitamfungua. Lakini wakatoa sauti zao kwa nguvu sana, wakitaka asulibiwe. Sauti zao zikashinda. Pilato akahukumu kwamba haja yao ifanyike. Akamfungua yule aliyetupwa gerezani kwa ajili ya fitina na uuaji, yule waliyemtaka, akamtoa Yesu wamfanyie watakavyo”.


Utangulizi:
Moja ya mambo ya kuyatafakari na kujiuliza kwa kina hususani katika wakati huu wa Pasaka ni pamoja na tabia ya wanadamu ambayo ni tabia ya kushangaza sana, tabia hii ngumu kuelezeka kwamba inatokana na woga, kutokujiamini, saikolojia ya mkumbo, kushindwa kusimama katika kweli, unafiki, au namna gani, hii ni ile tabia yetu ya kung’angania vitu vibaya, viovu na vyenye kuleta shida katika maisha yetu na kupoteza vitu vyema vizuri na vyenye thamani au vyenye kuleta ukombozi kutoka katika changamoto tulizonazo, Mwondoshe huyu, utufungulie Baraba! Haya yalikuwa maneno ya watu wote siku Mwokozi wa ulimwengu huu alipohukumiwa kusulubiwa kwa kura za wanadamu ambao kwa nia moja walitaka asulubiwe na mtu mhalifu zaidi aweze kuachwa huru!

Nani maarufu kati ya Yesu na Baraba?

Wote tunaweza kukubaliana wazi kuwa kifo cha Yesu Msalabani kilikuwa kina kusudi la Mungu nyuma yake, ilikuwa ni lazima Yesu asulubiwe ili mimi na wewe tuokolewe kutoka katika adhabu ya dhambi zetu sio mimi na wewe tu bali na hata watu waovu labda huenda kuliko mimi na wewe kama ilivyokuwa kwa Baraba

Kinachonishangaza hapa na amabachoi nataka kukijadili kwa kina ni sababu gani inapelekea watu wampuuzie Yesu kwa kiwango hata cha kutokutaja jina lake, na wakati huo huo wamchague mtu mhaini na muuaji Baraba kwamba awe huru huku akitajwa kwa jina lakini Yesu akitajwa kama huyu? Je wadhani Yesu na baraba ni nani alikuwa maarufu zaidi?

Biblia au neno la Mungu linatueleza wazi kuwa Yesu Kristo ndiye alikuwa mtu maarufu zaidi katika karne yake kuliko mtu awaye yote, Yeye aliandamwa na maelfu ya watu kila alikokwenda ili waponywe magonjwa yao na kusikiliza hekima yake na mafundisho yake na wengine wakitaka tu kumuona, nataka nikuwekee wazi kabisa kuwa haikuwa jambo rahisi kuweza kumfikia Yesu hata kwa karibu, Bibliainaeleza kuwa watu walipanda hata juu ya miti ili angalau waweze kumuona

Luka 19:2-4Na tazama, palikuwa na mtu, jina lake Zakayo, mkubwa mmoja katika watoza ushuru, naye ni tajiri. Huyu alikuwa akitafuta kumwona Yesu ni mtu wa namna gani, asiweze kwa sababu ya umati wa watu, maana ni mfupi wa kimo.  Akatangulia mbio, akapanda juu ya mkuyu apate kumwona, kwa kuwa atakuja kuipitia njia ile” unaweza kuona Biblia inaeleza kuwa huyu alikuwa mtu mkubwa, tena alikuwa tajiri nyakati za leo tungeweza kumfananisha mtu huyu kama alikuwa waziri wa fedha hivi, alitamani kumuona Yesu lakini ilikuwa ni ngumu sana, maelfu ya watu walikuwa wakimzingira Yesu pande zote alikuwa maarufu Yesu kuliko mtu yeyote,


Luka 5:19Hata walipokosa nafasi ya kumpeleka ndani kwa ajili ya lile kundi la watu, walipanda juu ya dari wakampisha katika matofali ya juu, wakamshusha yeye na kitanda chake katikati mbele ya Yesu.” Wako watu walikosa nafasi ya kumuona Yesu kiasi ambacho walitoboa dari ya nyumba ili angalau waweze kufikisha mgonjwa wao kutokana na Yesu kuzungukwa na umati mkubwa wa watu, Yesu alikuwamaarufu kuliko mtu awaye yote, wewena mimi hata tukipanda daladala hakuna hata mtu mmoja anashituka au kugeuka kukuangalia, kondakta anaweza hata kukuamboa brother adjust tuikae watano watano hapo kati, Hii haikuwa hivyo kwa Yesu alijulikana mno, Biblia imejaa mifano mingi na habari nyingi kuhusu Yesu kuzingirwa na umati wa watu wakihitaji huduma kutoka kwake.

Watu walimzunguka Yesu kiasi ambacho yeye na wanafunzi wake walikosa hata nafasi ya kula Marko 3:20Mkutano wakakusanyika tena, hata wao wenyewe wasiweze hata kula mkate.”
Yesu alizungukwa na watu pande zote wakati mwingine alilazimika kukaa katika chombo cha majini ili kila mmoja aweze kumuona alipokuwa akifundisha Marko 4:1Akaanza kufundisha tena kando ya bahari. Wakamkusanyikia mkutano mkubwa mno, hata yeye akapanda chomboni, akakaa baharini, mkutano wote ulikuwako juu ya nchi kavu kando ya bahari.
Yesu hata aliposafiri aliandamwa sio tu na wanafunzi wake lakini biblia inasema umati mkubwa wa watu walifuatana pamoja naye Luka 7:11 “Baadaye kidogo alikwenda mpaka mji mmoja uitwao Naini, na wanafunzi wake walifuatana naye pamoja na mkutano mkubwa”.
Yesu ndiye mtu pekee ambaye hata Mama yake na ndugu zake walipotaka kumuona walipata taabu saba kufikia kutokana na kuzongwazongwa na watu Luka 8:19 “Wakamwendea mama yake na ndugu zake, wasiweze kumkaribia kwa sababu ya mkutano.”
Yesu ndiye kiongozi pekee ambaye maelfu ya watu walikusanyika pamoja ili kumuona, alikuwa na mvuto mkubwa kiasi ambacho watu waliweza kukanyagana Luka 12:1a. “Wakati huo, makutano walipokutanika elfu elfu, hata wakakanyagana,aidha maandiko yanaeleza wazi kuwa umati mkubwa wa watu ulimfuata kila mahali alikokwenda watu walitoka uyahudi, Yerusalem, Idumeya, Yordani, Tiro na hata Sidoni yaani sehemu za Lebanon ya leo, wengine wakimfuata kutoka Galilaya

Marko 3:7-10 “Naye Yesu akajitenga, yeye na wanafunzi wake, akaenda baharini. Mkutano mkuu ukamfuata, kutoka Galilaya, na Uyahudi, na Yerusalemu, na Idumaya, na ng'ambo ya Yordani, na pande za Tiro na Sidoni, mkutano mkuu, waliposikia habari za mambo yote aliyokuwa akiyatenda, wakamwendea. Akawaambia wanafunzi wake ya kwamba chombo kidogo kikae karibu naye, kwa sababu ya mkutano, wasije wakamsonga. Maana aliponya wengi, hata wote waliokuwa na misiba wakamrukia wapate kumgusa.”
Luka 9:12 “Na jua likaanza kushuka; wakamwendea wale Thenashara, wakamwambia, Uage mkutano, ili waende katika vijiji na mashamba ya kandokando wapate mahali pa kulala na vyakula, maana hapa tulipo ni nyika tupu”.  Yesu aliandamwa na umati mkubwa wa watu ambao walikuwa hawataki kumuachia kundi hili kubwa sana la watu walishuhudia miujiza ya ajabu ya kihistoria walishuhudia pia wakilishwa mikate na Yesu kiasi cha kushibisha biblia inataka kuwa wanaume 5000 walilishwa bila kuhesabu wanawake na watoto, vilema waliponywa, vipofu walifunguliwa, pepo walitolewa, wafu walifufuliwa na miujiza mingine mingi ya kuwahudumia watu      Biblia inaeleza kuwa Nafasi isingeliweza kutosha kuelezea kila alilolifanya Yesu Yohana 21:25 “Kuna na mambo mengi aliyoyafanya Yesu; ambayo yakiandikwa moja moja, nadhani hata ulimwengu usingetosha kwa vile vitabu vitakavyoandikwa.”
Yesu aliwaponya wote walikuwa wanaumwa Mathayo 12:15, Alipowaona umati mkubwa wa watu waliokuwa kama kondoo wasio na Mchungaji aliwahurumia Mathayo 14:14 na umati mkubwa wa watu walimfuata kwa sababu waliona miujiza na ishara na jinsi alivyoponya wagonjwa Luka 19:37 lakini kama haiztoshi umati mkubwa sana ulikuwa pamoja naye alipomfufua lazaro Yohana 12:17  
Unaweza kupata picha na ushahidi wa kimaandiko namna na jinsi Yesu alivyokuwa mtu muhimu sana katika jamii, yeye hakuwa muhalifu, alizunguka huko na huko akiwahudumia watu na kuwahurumia na kuwaponya yeye alikuwa mwema sana katika maisha yao.

Kwa nini makutano walimchagua Baraba?

Swali linakuja sasa kwa nini Pilato alipowataka watu wayahudi hadharani kuchagua Mfungwa mmojawapo kati ya Yesu  mtenda miujiza na Baraba  muuaji watu walichagua tusichikidhani? Mbona ni kama jibu lilikuwa wazi sana lakini eti watu walijibu tena bila ya kumtaja jina Bwana Yesu kana kwamba hakuwa na faida yoyote kwao? Muondoshe huyu, tufungulie Baraba,
Uchaguzi huu wa watu unatuthibitishia wazi kuwa wakati huu Yesu hakuhesabika kuwa ni wa thamani kabisa, na alidharaulika na kutokuonekana kuwa kitu kwamkiwango ambacho baraba alionekana kuwa wa muhimu, umuhimu wa Yesu na Baraba kwa jamii ulikuwa na tofauti kubwa sana, wayahudi na jamii ya watu waliokuwepo sio tu kuwa walipiga kelele kuwa waachiwe Baraba lakini pia walionyesha wazi kuwa wanchukizwa na hawampendi kabisa Yesu Luka 23:23 inasema wazi kabisa kuwa walipiga kelele kwa nia moja wakisema Msulubishee msulubishee, hii inaonyesha wazi kuwa watu hawakuwa wamevutiwa na Yesu wala kazi zake
Hali halisi iliyokuwepo inaweza kukutoa Machozi kama tungekuwepo na sisi pale, tukiacha ujuzi kuwa Mungu alikuwa kazini kuwaokoa wanadamu na kuwafia wenye dhambi baraba akiwa mmoja wao, Lakini tujiulize je walikuwa wapi wale ambao kwa dhati kabisa walitemntewa mema na Yesu live? Liko wapi lile kundi lililokuwa likimfuata? Wako wapi wale waliokula mikate wakashiba na kutaka kumfanya kuwa mfalme?, je walishindwa kusema muachie Yesu kwa sababu mimi nilikuwa kipofu na sasa kwaajili yake ninaona? Wako wapi walemavu walioponywa? Wako wapi waliotolewa Pepo?, wako wapi walioponywa magonjwa yao? Wako wapi maakida ambao Yesu aliwaponya watumwa wao, yuko wapi mwanamke aliyekuwa akitokwa na damu na Yesu akamponya, yuko wapi Zakayo aliyetembelewa na Yesu Nyumbani kwake, yuko wapi Lazaro angeweza kusema mimi nilikuwa maiti siku nne huyu jamaa akanifufua, wako wapi wale waliomshangilia siku ya mitende na kutandaza nguo zao njiani na kuimba Hosana mwana wa Daudi?, yuko wapi yule aliyetolewa Jeshi kubwa la mapepo, wako wapi watu kutoka Galilaya, Yerusalemu, Dekapoli, Yudea, Tiro na Sidoni, Kama Yesu alikuwa akizxungukwa na watu mpaka anakosa nafasi ya kula ilikuwaje siku hii?
Hakuna mtu aliyemfikiri Yesu kuwa ni wa muhimu kwa wakati huu, Muimbaji mmoja wa kitanzania aliyeitwa Patric Balisidya aliimba akisema “ni mashaka ya hangaiko wema hawana maisha” akiwataja watu wema ambao walikuwa wema kwa watu wao lakini hata hivyo waliuawa dunia imejawa na chuki na wivu na ndiyo yaliyoipamba dunia, wema wamepakwa majivu wala hawaonekani, je itakuwaje kizazimkile wakifufuka na kuona leo Majengo makubwa yakiwa yamejengwa na watu wakimuabudu Yesu, au wakiona watu waliokuwa waovu kuliko baraba wakiwa wamebadilishwa kabisa kitabia wangesemaje? Wangesema wao walikuwepo na kuwa sisi leo tumechagua vibaya?

Mwondoshe huyu, utufungulie Baraba.!

Swali bado linabaki kwa nini umati huu haukumtetea Yesu, ukiachilia zile sababu za kiroho kuwa ni ili mapenzi ya Mungu ya kuwaokoa wenye dhambi yaweze kutimizwa? Kuna ukweli ulio wazi kibiblia kwamba chuki hii ilipandwa, chuki hii ilikuwa ni mbegu iliyopandwa kutoka kwa viongozi wa dini, chuki ni mbegu mbaya, mbegu mbaya kwa kawaida hustawi haraka na kwa nguvu zaidi kiasi cha kuweza kuharibu jamii, ilichukua muda mfupi sana wanyarwanda kuuana kwa mamia na maelfu kwa sababu tu mbegu ya chuki ilipandwa, mbeguu hii ya chuki ilipandwa na adui ilipandwa na shetani kupitia viongozi wa kidini  biblia inaweka wazi kuwa wao ndio waliowashawishi makutano  wamchague baraba Mathayo 27:20 biblia inasema “ Nao wakuu wa makuhani na wazee WAKAWASHAWISHI makutano ili wamtake Baraba, na kumwangamiza Yesu.”  Unaweza kuona pia katika Marko 15:11Lakini wakuu wa makuhani WAKAWATAHARAKISHA makutano, kwamba afadhali awafungulie Baraba.
Maandiko yanaonyesha kuwa chuki dhidi ya Yesu ilipandwa tu, ilikuwa ni mbegu kutoka kwa shetani, ilipandikizwa dhidi ya Yesu viongozi hawa wa dini walikuwa ni maadui wa Yesu, walipinga kila alichokuwa akikifanya, walipanga mipango ya kumuua, walitafuta makosa hata ya kutunga kwaajili yake, walitaharakisha na kuwachochea makutano wachague lililo ovu, wakati wote tunapoona watu wakitenda maovu ni lazima uelewe kuwa kuna mchochezi, alisema Sulemani kuwa moto hauwezi kuwaka pasipo kuchochewa kwa kuni, Mungu alikuwa amewapiga upofu kuchagua uovu na kukataa wema Yesu alikuwa amekwisha kuwaonya mbeleni kuwa ikiwa wameutendea vile mti mbichi itakuwaje kwa mti mbichi?
Inasikitisha kuwa watu waliacha kumuamini Yesu na waamini uongo, waliacha kumuamini mtenda miujiza wakaamini viogozi vipofu wa kidini, Mbegu ya chuki inapoingia katika eneo lolote lile hata kutaja jina lako inakuwa shida Yesu sasa anatajwa kama “huyu” mwondoshe huyu! Tufungulie Baraba
Ni wazi kabisa hata katika jamii leo watu wanaamua kuchagua njia mbovu na kuacha kuacha njia njema, leo ukisimama kupinga uovu na kuwashauri watu wema unaonakana kama adui,watu wenye akili leo na walioendelea wanapiga kura kuchagua uovu na kupitisha uovu huku wakiwa na majina yanayoashiria kuwa wao ni wa upande wa Mungu?  Katika wakati huu wa pasaka ni muhimu kila moja kujiuliza nani aondoshwe na nani afunguliwe! Nakushauri muondoshe Baraba katika maisha yako na mfungulie Yesu kristo mlango katika moyo wako
Yeye aliahidi kuwa anagonja na mtu akifungua ataingia kwake na kukaa naye Pasaka hii mkaribishe Yesu na mfukuze baraba katika maisha yako, usikubali kuangalia umati wa watu wanasemaje na wana maoni gani wewe simama umtetee Yesu hadharani.
Rev. Innocent Kamote
Mkuu wa wajenzi mwenye Hekima.

Jumatano, 27 Machi 2019

Mungu aonaye!


Mwanzo 16:1-13 “Basi Sarai mkewe Abramu hakumzalia mwana, naye alikuwa na mjakazi, Mmisri, jina lake Hajiri. Sarai akamwambia Abramu, Basi sasa, BWANA amenifunga tumbo nisizae, umwingilie mjakazi wangu labda nitapata uzao kwa yeye. Abramu akaisikiliza sauti ya Sarai. Sarai mkewe Abramu akamtwaa Hajiri Mmisri mjakazi wake, baada ya kukaa Abramu katika nchi ya Kanaani miaka kumi, akampa Abramu mumewe, awe mkewe. Basi akamwingilia Hajiri, naye akapata mimba. Naye alipoona ya kwamba amepata mimba, bibi yake alikuwa duni machoni pake. Sarai akamwambia Abramu, Ubaya ulionipata na uwe juu yako; nimekupa mjakazi wangu kifuani mwako, naye alipoona kwamba amepata mimba, mimi nimekuwa duni machoni pake. BWANA na ahukumu kati ya mimi na wewe. Naye Abramu akamwambia Sarai, Tazama, mjakazi wako yu mkononi mwako, mtendee lililo jema machoni pako. Sarai akamtesa, naye akakimbia kutoka mbele yake. Malaika wa BWANA akamwona kwenye chemchemi ya maji katika jangwa, chemchemi iliyoko katika njia ya kuendea Shuri. Akamwambia, Hajiri, wewe mjakazi wa Sarai, unatoka wapi, nawe unakwenda wapi? Akanena, Nakimbia mimi kutoka mbele ya bibi yangu Sarai. Malaika wa BWANA akamwambia, Rudi kwa bibi yako, ukanyenyekee chini ya mikono yake. Malaika wa BWANA akamwambia, Hakika nitauzidisha uzao wako, wala hautahesabika kwa jinsi utakavyokuwa mwingi. Malaika wa BWANA akamwambia, Tazama! Wewe una mimba, utazaa mwana wa kiume, nawe utamwita jina lake Ishmaeli, maana BWANA amesikia kilio cha mateso yako. Naye atakuwa kama punda-mwitu kati ya watu, mkono wake utakuwa juu ya watu wote na mkono wa watu wote utakuwa juu yake, naye atakaa mbele yao ndugu zake wote. Akaliita jina la BWANA aliyesema naye, Wewe U Mungu uonaye, kwani alisema, Hata hapa nimemwona yeye anionaye?”


Utangulizi:

Ni muhimu kwa kila mwanadamu kuwa na ufahamu kwamba kila wakati tunapopitia Mateso na mambo  magumu ya kukatisha tamaa, kukumbuka kuwa hatuko wenyewe, Mungu aonaye “Jehoha Rohi” anaona kila tunalolipitia na kila kinachotokea katika maisha yetu, Mungu anajali sana  na anajishughulisha sana na mambo yetu, Yeye sio mwepesi wa hasira, wala sio Mungu aliye mbali, au asiyejali yeye anajali, anatamani sana tuwe na mambo mazuri na kila kitu kituendee vizuri katika maisha yetu, anataka kila mmoja wetu aweze kuwa na maisha ya ushindi na furaha, sisi ni watoto wake ni kondoo wa malisjo yake anawajibika kututunza na kushughulika na mahitaji yetu Bila upendeleo.

Mungu anajua na anaona kila unachopitia.

Mwanzo 16:1-6Basi Sarai mkewe Abramu hakumzalia mwana, naye alikuwa na mjakazi, Mmisri, jina lake Hajiri. Sarai akamwambia Abramu, Basi sasa, BWANA amenifunga tumbo nisizae, umwingilie mjakazi wangu labda nitapata uzao kwa yeye. Abramu akaisikiliza sauti ya Sarai. Sarai mkewe Abramu akamtwaa Hajiri Mmisri mjakazi wake, baada ya kukaa Abramu katika nchi ya Kanaani miaka kumi, akampa Abramu mumewe, awe mkewe. Basi akamwingilia Hajiri, naye akapata mimba. Naye alipoona ya kwamba amepata mimba, bibi yake alikuwa duni machoni pake. Sarai akamwambia Abramu, Ubaya ulionipata na uwe juu yako; nimekupa mjakazi wangu kifuani mwako, naye alipoona kwamba amepata mimba, mimi nimekuwa duni machoni pake. BWANA na ahukumu kati ya mimi na wewe. Naye Abramu akamwambia Sarai, Tazama, mjakazi wako yu mkononi mwako, mtendee lililo jema machoni pako. Sarai akamtesa, naye akakimbia kutoka mbele yake.”

Katika kifungu cha maandiko wote tunaweza kuoina hali halisi, iliyojiyokeza katika familia ya Ibrahimu na Sara a mjakazi wao Hajiri, kwamba japo jambo hili lilikuwa sawa katika mila na desturi za kikaldayo, lakini haikuwa sawa katika macho ya Mungu, ziko mila na desturi ambazo watu baada ya kuwa na urafiki na Mungu wakizifuata zinaweza kuharibu mtiririko wetu wa imani katika kuonyesha kuwa tunamtegemea Mungu, Sara alikuwa amechoka kwa mapito aliyokuwa akiyapitia, Mungu alikuwa amemuona Sara na alikuwa amekwisha kumuahidi kuwa atamkumbuka lakini Sara alikuwa ameelemewa na huzuni na maumivu:-

·         Maumivu yamatumaini yaliyokuwa yakitarajiwa lakini yamechelewa
·         Maumivu yanayoashiria kana kwamba Mungu hajajibu mamombi au amechelewa kujibu maombi
·         Maumivu kwamba mikono yake haijawahi kushika mtoto wake mwenyewe
·         Maumivu ya aibu kujulikana kama mwanamke aliye tasa au mgumba na asiyezaa katika jamii
·         Maumivu ya kumlaumu Mungu kama asiyejali maumivu yake na mateso yake

Hali hii inampelekea Sara kuamua kutumia akili na njia za kibinadamu kutatua tatizo walilonalo katika familia yake, Usahwishi wake kama ilivyokuwa kwa Eva na Adamu unasikilizwa na Ibrahimu, wanaamua kuongeza mke ambaye ni Hajiri, Bila shaka ni moja ya watumwa (Kijakazi) wa Sara  aliyepewa huko Misri na Farao, Matumizi yao ya akili katika kutaka kutatua tatizo lao nje ya mfumo wa njia za kimungu kunaleta tatizo kubwa zaidi, Hajiri anashika Mimba, lakini yeye sasa anapoteza kutii, kule kushika Mimba kunampa kiburi, anasahaku kuwa aliinuliwa kwa mawazo ya Sara, mgogoro unakuwa mkubwa sara anaona Abrahamu kuwa pia ni sehemu ya tatizo, Abrahamu anamuonyesha sara kwamba hajiri bado ni mtumwa wake ni mjakazi wake anaweza kumfanya anachokitaka, sasa sara anamtesa Hajiri, huku Ibarahimu akiwa ameridhia kuteseka kwa Hajiri, mwanamke huyu mnyonge, na masikini sasa hana namna kibano kimezidi kuwa kikali sana na sasa anakimbia jangwani, Ni safari ngumu, ni safari ndefu, bila shaka alikuwa akijaribu kurejea kwao Misri lakini bila msaada wa wowote, hakuna anayejali wala hakuna anayetaka kubeba lawama kila mtu amechoka. Ni mwanamke mjamzito, anataka kiujaribu kurudi kwao, kupitia Jangwani, hana msaada kuna wanyama wakali, kilichoko kwenye kichwa chake “NI HERI KUFA KULIKO MATESO NINAYOYAPITIA KWA SARA” Biblia haijaeleza kuwa sara alimfanya nini lakini mwanatheolojia mmoja ametumia neno la Kiingereza “Sarai attacked Hagar with disproportionate cruelty,” Neno hilo “DIS-PRO-POR-TIONATE” maana yake ukatili usiopimika, na maneno mengine ya kiingereza “Harshly, Cruel, severe, Mistreated   ni aibu kwa mwanamke bosi kama Sara kuwa na ukatili wa aina ile ni aibu, japo haikuwa vema pia kwa Hajiri kuwa asiyetii, lakini hali hizi zote ziliweza kufikisha katika hatua hii, wako watu duniani wanajua kutesa, wako watu duniani wanajua kunyanyasa mpaka inapofikia hatua ya mtu kuchagua kujiua kuliko mateso unayoyapata, Mungu sio mjinga, Mungu sio kipofu, Mungu sio Mungu asiyejali, Mungu sio Mungu wa Upendeleo, Mungu ni Mungu aonaye, Hajiri anakuwa ni Mwanamke wa kwanza Duniani kumuona malaika wa Bwana, Hajiri anajulikana Mbinguni, Mungu anamtaja kwa jina lake… Munguanamjua anakotoka na anakokwenda Hajiri ni mwanamke wa Kwanza  kumpa Mungu Jina “YEHOVAH ROHI” alishuhudia kuwa Mungu alimuona.

Mungu ataingilia kati hali unayoipitia.
Mwanzo 16:7-13Malaika wa BWANA akamwona kwenye chemchemi ya maji katika jangwa, chemchemi iliyoko katika njia ya kuendea Shuri. Akamwambia, Hajiri, wewe mjakazi wa Sarai, unatoka wapi, nawe unakwenda wapi? Akanena, Nakimbia mimi kutoka mbele ya bibi yangu Sarai. Malaika wa BWANA akamwambia, Rudi kwa bibi yako, ukanyenyekee chini ya mikono yake. Malaika wa BWANA akamwambia, Hakika nitauzidisha uzao wako, wala hautahesabika kwa jinsi utakavyokuwa mwingi. Malaika wa BWANA akamwambia, Tazama! Wewe una mimba, utazaa mwana wa kiume, nawe utamwita jina lake Ishmaeli, maana BWANA amesikia kilio cha mateso yako. Naye atakuwa kama punda-mwitu kati ya watu, mkono wake utakuwa juu ya watu wote na mkono wa watu wote utakuwa juu yake, naye atakaa mbele yao ndugu zake wote. Akaliita jina la BWANA aliyesema naye, Wewe U Mungu uonaye, kwani alisema, Hata hapa nimemwona yeye anionaye”

Unaweza kuona tayari hali ya Hajiri ilishaanza kuwa mashakani, ashukuriwe Mungu alikuwa amekwama kwenye kisima cha maji jangwani, kwa vyovyote vile hapo alipumzika kama angeendelea mbele hali ya hatari ilikuwa ikimkabili, Jangwa la shuri ni jangwa pan asana unapoliangalia huwezi kuna mwisho waka ukigeuka huwezi kuona utokako hii ilikuwa ni muelekeo wa kuangamia sasa kwa mwanamke kijana tena mwenye mimba alihitaji msaada na sasa Bwana mwenyewe anamtokea angalia maneno ha malaika wa Bwana:-

-          Wewe Hajiri Mjakazi wa Sarai
-          Unatoka wapi nawe unakwenda wapi
-          Rudi kwa bibi yako ukanyenyekee chini ya mikono yake
-          Nitauzidisha uzao wako wala hautahesabika kwa jinsi utakavyouwa mwingi
-          Utazaa mtoto wa kiume nawe utamwita Ishamel maana Bwana amesikia kilio cha Mateso yako
-          Atakuwa kama punda mwitu, atakaa mbele ya ndugu zake wote
-          Mkono wake utakuwa juu ya watu wote na mkono wa watu wote utakuwa juu yake.

Malaikia wa bwana alionyesha kuwa anamjua Hajiri vizuri sana kwa jina lake na kwa kazi yake, Malaika wa bwana alitaka kupima unyenyekevu ndani ya hajiri kwamba anajisikiaje kuitwa Mjakazi wa Sarai, Swali unatoka wapi na unakwenda wapi lilikuwa lina kusudi la kumrejesha Hajiri,katika toba na kuacha kiburi, kisha kurudi panapopaswa na kuwa Mnyenyekevu , kwa sababu kwa mila na tamaduni alikuwa na mtoto wa watu hao tumboni, na hivyo alipaswa kumrejesha, alimuakikishia kuwa uzao wake utakuwa mwingi, maneno haya huenda yalikuwa ni maneno aliyozoea kuyasikia katika familia ya Ibrahimu kuhusu ahadi za Mungu, ni wazi maneno hayo na ahadi hizo zilimfanya hajiri awe na utambuzi kuwa huyu hakuwa malaika wa bwana tu bali alikuwa ni Mungu mwenyewe alikuwa na ujuzi kuwa Mungu anaona, ujuzi huu una umuhimu mkubwa kwetu, Mungu mwenye kuhusika na mahitaji ya wanadamu anaona na anajua kila kitu na kila njia na aina ya mateso tunayoyapitia.

Hakuna mtu mwenye hati miliki ya Mungu, Mungu sii wa Ibrahimu na Sara tu, wala Mungu si wa matajiri peke yao, Mungu ni wa kila mtu, anajali na anamuhurumia kila mtu bila kujali kabila wala rangi yake, inapofikia ngazi ya kukata tamaa yuko Mungu anayesikia na kuona mateso yetu, yuko Mungu anayejua sida na mateso na changamoto unazozipitia, yeye atahusika na maisha yako, hana dini wala ukabila hana upendeleo, kila mtu anayemwendea na kuliitia jina lake anasikiwa, anaweza kumuongeza na kumzidisha awaye yote, hakuna mtu maalumu kwa Mungu, Mungu ni wa watu wote, Mungu anataka kumponya na kumganga na kumuhudumia kila mmoja wetu, Unaweza kuteswa, kunyanyaswa, kuonewa na kufanyiwa mabaya lakini liko Jicho lenye nguvu linalochungulia ulimwenguni na kuitafuta haki ili kuona ikitendeka na kama haitendeki, huingilia kati na kutokezea njia yeye ni Mungu aonaye

Kutoka 3:7-9BWANA akasema, Hakika nimeyaona mateso ya watu wangu walioko Misri, nami nimekisikia kilio chao kwa sababu ya wasimamizi wao; maana nayajua maumivu yao; nami nimeshuka ili niwaokoe na mikono ya Wamisri, niwapandishe kutoka nchi ile, hata nchi njema, kisha pana; nchi ijaayo maziwa na asali; hata mahali pa Mkanaani, na Mhiti, na Mwamori, na Mperizi, na Mhivi, na Myebusi. Basi, tazama, kilio cha wana wa Israeli kimenifikilia; tena nimeyaona hayo mateso ambayo Wamisri wanawatesa.

Mungu aonaye Jehovah Rohi macho yake yako kila mahali hawezi kuvumilia kuona unateseka mpaka unalia na kuugua au kuchagua kufa kuliko kuishi, wakati mateso yako yanapozidi kupita uwezo wako, wakati mateso yako yanapokaribia kukutupa nje, unapokata tamaa ya kuishi kumbuka kuwa Mungu kupitia mwanaye Yesu ambaye ni Mwokozi atakutetea atashuka na kuingilia kati na kukurejesha kwenye furaha yako nawe utasimulia matendo yake makuu nimemuona yeye aonaye.
Na. Rev. Innocent Kamote.
Mkuu wa Wajenzi mwenye Hekima.

Alhamisi, 21 Machi 2019

Mtu atakayelitengeneza boma !



Ezekiel 22:30-31.Nami nikatafuta mtu miongoni mwao, atakayelitengeneza boma, na kusimama mbele zangu mahali palipobomoka, kwa ajili ya nchi, nisije nikaiharibu, lakini sikuona mtu. Kwa sababu hiyo nimemwaga ghadhabu yangu juu yao; nimewateketeza kwa moto wa hasira yangu; nami nimeileta njia yao wenyewe juu ya vichwa vyao, asema Bwana MUNGU.”




Utangulizi:

Ni muhimu kufahamu kuwa Mungu katika mpango wake wa ukombozi, hapendi kufanya mambo duniani bila kuwahusisha wenyeji wa dunia, Mungu huwa anatafuta mtu ili aweze kumtumia katika kuujenga ufalme wake, inapotokea kuwa Familia, ukoo, jamii au hata taifa limemtenda Mungu dhambi ni wajibu wa Mungu, kuikemea, kuonya na hata kuhukumu wale waliofanya uovu, hata hivyo Kabla ya Mungu kuhukumu pia huwa anatafuta mtu, ili yamkini aweze kumtumia mtu huyo kutoa Maonyo ili kwamba kama watu watatubu aweze kuwasamehe, hii ni kwa sababu yeye pia ni mwingi wa huruma na neema.

Ezekiel 22:30-31.Nami nikatafuta mtu miongoni mwao, atakayelitengeneza boma, na kusimama mbele zangu mahali palipobomoka, kwa ajili ya nchi, nisije nikaiharibu, lakini sikuona mtu. Kwa sababu hiyo nimemwaga ghadhabu yangu juu yao; nimewateketeza kwa moto wa hasira yangu; nami nimeileta njia yao wenyewe juu ya vichwa vyao, asema Bwana MUNGU.”

Katika kifungu hiki ambacho tunachukua Muda kujifunza leo, Tunaona Mungu akimueleza Mtumishi wake Ezekiel sababu za kuhukumiwa kwa utawala ya Yuda, na kufikia hatua ya Mungu kuliharibu taifa na hata kuruhusu vita na wao kuchukuliwa Mateka ni kwamba taifa lilipoteza watu wenye haki na waombezi, na waonyaji na wale waliokuwa na ushawishi wa kumuomba Mungu kwaajili ya watu hata Mungu akasikia.

A.     Hali ya taifa zima ilikuwa ni hali ya dhambi na watu walikuwa wameharibika

1.      Viongozi wa serikali walikuwa wameharibika sana
a.      Walifanya ufisadi na kupokea rushwa
b.      Makunani nao walikuwa wamejiingiza katika anasa za dunia na kuacha utumishi wao
c.       Watu wengi wa Mungu walijishughulisha na utafutaji mali, wakitafuta mali za ulimwengu
d.      Maswala ya ibada yalionekana kuwa ni ushamba, na kupoteza muda
e.      Walilitafasiri neno la Mungu kwa kusudi la kupata hekina na sio kuliamini
f.        Manabii wengi walikuwa hawakemei uovu bali waliwatabiria watu amani amani
g.      Walitabiri ushindi hata pale ambapo watu walikuwa wameshindwa vibaya kiroho
h.      Walitabiri amani wakati Mungu alikuwa amekusudia vita na hukumu
i.        Waliwatabiria watu kuwa na mali wakati Mungu alikusudia wawe mateka
j.        Watu walikosa Muongozo wa kiroho na walikuwa waliangukia katika 

B.      Mungu alikuwa anatafuta mtu atalayelitengeneza Boma na kusimama mahali palipobomoka

1.      Mungu ni mwingi wa rehema na neema angeweza kuwasamehe endapo angepatikana mtu wa kusimama mahali palipobomoka na kulitegeneza boma Yeremia 15:1Ndipo Bwana akaniambia, Hata wangesimama mbele zangu Musa na Samweli, moyo wangu usingewaelekea watu hawa; watupe, watoke mbele za macho yangu, wakaende zao.Mungu aliwakumbuka watu wenye haki walioweza kudumisha uhusiano wao na Mungu kiasi ambacho Mungu aliweza kuwasikiliza walipofanya maombezi kwaajili ya taifa na Mungu akasikia dua zao mfano Musa na Samuel, lakini kwa vile hakuona watu wa kiwango hicho aliweza kuwahukumu watu wake.

a.      Mungu hakupata watu au mtu wa kulitengeneza Boma, katika lugha ya kiingeza neno boma linasomeka kama “HEDGE” hii ni aina ya miti au maua magumu yaliyotumika kupandwa shambani au nyumbani kwa kusudi la kuweka uzio ili kuzuia uvamizi na uharibifu kwa mazao au uvamizi nyumbani au katika makazi yaliyokusudiwa kulindwa.

b.      Watu wanapofanya dhambi uzio huo unakuwa umebomoka katika ulimwengu wa roho na unaweza kuruhusu Hasira za Mungu kupita na kufanya uharibifu kwa hiyo ni lazima awepo MUOMBEZI, mtu atakayelia na kuomboleza kwaajili ya kuwaombea watu rehema kwa Mungu, ni aina hii ya watu ndio Mungu anawatafuta hapa Katika Yuda Mungu hakuwaona hao.

i.    Watu walikuwa busy na ujenzi wa makazi yao
ii.  Watu walikuwa wakijiimarisha kutafuta nguvu za kiuchumi na kujiongezea mapato
iii.Watu walijishughulisha na Mashamba yao, vyote havikuwa vitu vibaya lakini vitakuwa na faida gani kama Mungu ataruhusu Moto na uharibifu wa hukumu yake usambaratishe hayo yote na kwa kweli vilisambaratishwa.
c.       Mungu hakuona mtu na kwa sababu hiyo aliruhusu uharibifu kuiharibu Israel.

Hitimisho.

Ni muhimu kufahamu kuwa wanapokuwepo watu ambao Mungu anawaheshimu kwa kiwango cha Musa watu hao wana ushawishi mkubwa wa kuweza kumuomba Mungu au kumsihi Mungu kubadili maamuzi yake, Mara kadhaa Mungu alikusudia kuwafutilia Mbali wana wa Israel Pale walipomuudhi lakini Musa alisimama kwa nguvu na kumwambia Mungu HAPANA angalia  Zaburi 106:23 “Akasema ya kuwa atawaangamiza Kama Musa, mteule wake, asingalisimama, Mbele zake kama mahali palipobomoka, Ili aigeuze hasira yake asije akawaharibu.” Mungu anatafuta viongozi wa Kisiasa, viongozi wa dini na watu wacha Mungu watakaodumisha uhusiano wake na yeye na kuleta mapinduzi makubwa ya kijamii, kiroho na mabadiliko makubwa na kusababisha watu wamche Mungu na kumgeukia yeye, watakaoleta uamsho, wakataokomesha ufisadi, na kuifanya taifa kutembea katika uadilifu, Mungu anatafuta waombaji, watu watakaosimama kumshawishi aisamehe Familia, ukoo wako, taasisi yako kijiji chako na wilaya yako mkoa na taifa, wakikosekana watu wenye ushawishi wa iana hii katika Taifa lazima hasira ya Mungu itashuka na hukumu kubwa itafuata, Kama taifa halina viongozi wa kiserikali, waombaji na makuhani na manabii wanachekelea dhuluma ikifanyika, mizani zikivurugwa, haki zikipindishwa taifa lazimalitaanguka tu, Haki huinua taifa bali dhambi ni aibu ya watu wote, Hatuna budi kuhakikisha kuwa tunasimama katika zamu yetu kwa haki na kuliombea taifa.

Ni aibu Mungu kukosa waombaji, Mungu anapokosa waombaji katika jamii anaibomoa jamii hiyo na kuisambaratisha, anakuwa hana namna nyingine zaidi ya kuihukumu, Mungu anatoa wito wa watu kurudi magotini, kuomba kwa siri na kuwa watu wenye kuiombea jamii na taifa, watu wengi waombaji wametoweka Duniani leo na mambo yanakwenda Kombo, Mungu anatafuta mtu atakayesimama mahali palipobomoka na kulitengeneza Boma ili asiharibu Nchi.

*Rev. Innocent Kamote*
*Mkuu wa wajenzi Mwenye Hekima*.