Jumatatu, 16 Septemba 2019

Mungu na wakimbizi:

Ni muhimu kufahamu kuwa kuwahudumia wakimbizi ni mpango wa Mungu!, Leo tutachukua Muda wa kutosha kwa kina na upana na urefu kuangalia huduma muhimu kwaajili ya wakimbizi Duniani, Mwaka 2004 pekee karibia watu milioni tatu na nusu walikuwa ni wakimbizi barani Afrika pekee, ambao walikimbia na kuishi nje ya nchi zao, na wengine zaidi ya milioni kumi walikuwa ni wakimbizi ndani ya nchi zao, wengi walikuwa hawakimbii tumatukio ya majanga ya kiasili nlakini walikuwa wanakimbia matatizo ya kisiasa, ugomvi wa kimadaraka, matatizo ya kidini, ukabila na maswala mengineyo je neno la Mungu linasema nini kuhusu wakimbizi, kanisa limewahi kutafakari nini kuhusu wakimbizi? Tutajifunza somo hili kwa kuzingatia vipengele vitatu vifuatavyo:-


·         Neno la Mungu na wakimbizi
·         Mungu anawajali wakimbizi
·         Wakimbizi na mafundisho ya agano jipya

Neno la Mungu na wakimbizi:

Biblia inatambua kuweko kwa watu ambao wamewahi kukimbia huko na huko mbali na Nchi zao, kaini alikuwa mtu wa kwanza kufahamu madhara ya ukimbizi Mwanzo 4:12,”Utakapoilima ardhi haitakupa mazao yake, utakuwa mtoro na mtu asiye na kikao Duniani” Neno utakuwa mtoro ni sawa na utakuwa mkimbizi. Yakobo na Familia yake waliishimaisha ya ukimbizi kutokana na majanga ya njaa nchini kwao Mwanzo 47:3-4, “Farao akawauliza hao nduguze Kazi yenu ni nini? Wakamwambia Farao, Tumekuja kukaa ugenini katika nchi hii, kwa sababu wanyama wa watumwa wako hawana malisho, maana njaa ni nzito sana katika nchi ya kanaani, Basi twakusihi uturuhusu sisi watumwa wako tukae katika nchi ya gosheni” Yesu pia alikuwa mkimbizi huko Misri kwaajili ya kuokoa Maisha yake yaliyokuwa yakitafuta na mfalme Herode Mathayo 2:13-14. “Na hao walipokwisha kwenda zao tazama malaika wa Bwana alimtokea yusufu katika ndoto, akasema  Ondoka umchukue mtoto na mama yake , ukimbilie Misri, ukae huko hata nikuambie kwa maana Herode anataka amwangamize, Akaondoka akamchukua mtoto na mama yake usiku akaenda zake Misri” ziko sababu mbalimbali na mazingira ya aina mbalimbali yanayoweza kusababisha kila mmoja wetu kuwa mkimbizi kwa namna moja ama nyingine.

Mungu anawajali wakimbizi

Biblia iko wazi kuwa Mungu anawajali wakimbizi, alionyesha kujalia sana maisha ya Kaini hata pamoja na kuwa ukimbizi wake ulisababishwa na makosa yake mwenyewe Mwanzo 4:15. Mungu alimwambia Musa katika Torati kuandaa miji ya makimbilio kwaajili ya wakimbizi watakaokimbilia kutokana na sababu mbalimbali ama ambao watu wangelikuwa wanatafuta kuwaua, Kutoka  21:12-14, Hesabu 35:9-34, Mstari 10-13 inasema hivi  Nena na wana wa Israeli, uwaambie, Mtakapovuka mto wa Yordani na kuingia nchi ya Kanaani,Ndipo mtajiwekea miji iwe miji ya makimbilio kwa ajili yenu; ili kwamba mwenye kumwua mtu, pasipo kukusudia kumwua, apate kukimbilia huko.Na hiyo miji itakuwa kwenu kuwa makimbilio, kumkimbia mwenye kutwaa kisasi, ili asiuawe mwenye kumwua mtu, hata atakaposimama mbele ya mkutano ahukumiwe. Na hiyo miji mtakayowapa itakuwa kwenu ni miji sita ya makimbilio”.  Kumbukumbu 4:41-43, 19:3-13, Nyakati 6:42-55. Mungu aliagiza pia kuwa wageni walioambatana na Israel pia wanahitaji kuheshimiwa kimsingi tunapaswa kuwajali aina zote za wakimbizi waliokimbia nchi zao kwa sababu zozote zile ziwe za kisiasa, vita uchumi njaa  na ugumu mwingine wote wanapaswa kuheshimiwa kuhifadhiwa kutunzwa vizuri, kupendwa na kuhifadhiwa,kwa heshima na usawa sawa na raia wengine tukiwahesabu kuwa ni ndugu na jamaa zetu Walawi 25, Isaya 16:1-4, Ezekiel 47:21-23 Lawi 19:33-34. Isaya 16: 3-4 inasema “Lete shauri; kata neno; fanya kivuli chako kuwa kama usiku kati ya mchana; wafiche waliofukuzwa; usiwachongee waliopotea. Watu wangu waliofukuzwa waache wakae pamoja nawe; katika habari za Moabu, uwe sitara kwake mbele ya uso wake anayeharibu; maana yeye atozaye kwa nguvu amekoma; afanyaye ukiwa ametoweka; waliokanyaga watu wametoka katika nchi.”  

         
Wakimbizi na mafundisho ya agano jipya

Agano jipya linasisitiza sana kuwahudumia wageni kuwapenda na kuwajali wenye mateso na masikini Mathayo 25:35-40,  kwa maana nalikuwa na njaa, mkanipa chakula; nalikuwa na kiu, mkaninywesha; nalikuwa mgeni, mkanikaribisha; nalikuwa uchi, mkanivika nalikuwa mgonjwa, mkaja kunitazama; nalikuwa kifungoni, mkanijia. Ndipo wenye haki watakapomjibu, wakisema, Bwana, ni lini tulipokuona una njaa, tukakulisha, au una kiu tukakunywesha? Tena ni lini tulipokuona u mgeni, tukakukaribisha, au u uchi, tukakuvika? Ni lini tena tulipokuona u mgonjwa, au kifungoni, tukakujia? Na Mfalme atajibu, akiwaambia, Amin, nawaambia, kadiri mlivyomtendea mmojawapo wa hao ndugu zangu walio wadogo, mlinitendea mimi”. tofauti ya ndugu na wakimbizi iliondolewa kabisa katika agano jipya Yohana 13:34 kutokana na umoja wa waamini Yohana 17:20-23 na kutokana na udugu na wote kuwa wanafunzi wa Yesu Kristo.

Hivyo ni muhimu kwa kanisa kujihusisha na kuwahudumia wakimbizi punde linapotokea swala la wakimbizi na kukutana na mahitaji yao ya muhimu haraka , kama usalama, upendo, chakula mavazi, malazi, maji safi,madawa, Kumbuka kuwa Yesu atakuja kubagua Kondoo na mbuzi kwa misingi ya namna tunavyowajudumia wengine au wenye uhitaji Mathayo 25:31-46, bila huduma hizi ni vigumu kwa wakimbizi kuikubali injili, wanyarwanda wana usemi usemao “Inda irimo ubusa ntigira amatwi” yaani tumbo tupu halina masikio, Ni muhimu kanisa likakumbuka hilo likakumbuka kuwahubiri injili lakini pia kusikiliza injili kutoka kwao ikiwa wanauwezo wa kuhudumu ili kuwalea na kukuza huduma zao punde warudipo au kuwa wamisionari katika taifa letu, hivi ndivyo nyakati za kanisa la kwanza walivyofanya pia Matendo 8;1-4, 18:1-2, Hali hii itainua heshima yao na kuwatia moyo, kanisa pia linapaswa kufanya kitu cha ziada sio tu kuwaletea maji katika birika bali kuwaelekeza namna wanavyoweza kuchimba visima wenyewe ili kujipatia maji, kanisa linapaswa pia kujihusisha katika swala zima la kuangalia chanzo cha ukimbizi na kukishughulikia hii ina maana kuwa kanisa linapaswa kujishughulisha na swala la kufanya upatanisho na kutafuta majibu ya matatizo ili kuyatatua na watu waweze kurejea katika nchi zao kwa amani badala ya kuiacha kazi hiiikafanywa na serikali zaidi, Kanisa ni lazima lisimamie demokrasia, Haki, upatanisho na mswala ya uongozi kwa ujumla, unaweza kufikiri kuwa kazi hii ni ya kiserikali zaidi nay a kijamii zaidi kuliko ya kiroho, lakini nataka nikuambie kuwa ni ya Kiroho zaidi na inapaswa kanisa kuwa sambamba na mashirika ya kiserikali na yasiyo ya kiserikali yanayojihusisha na huduma kwa wakimbizi

Ni muhimu kuwahudumia vema wakimbizi wao pia ni binadamu, kuna historia za kutisha kuwa sehemu nyingine wakimbizi wanabakwa, wanakataliwa, wanawekewa uzio, au wanafanyiwa hila wafe,n.k. hivi karibuni katika nchi ya Syria kutokana na vita kumekuwa na wakimbizi wengi wanaokimbilia ulaya na wengine wanapitia Libiya lakini wengi wamefanyiwa hila wakikimbia kuokoa maisha yao wengine wameuawa na mataifa mengine yameingia hofu ya kuwapokea Mungu isaidie Dunia kuwa mahali panapofaa kukaa ni wajibu wetu kupiga vita kila kinachosababisha watu kukimbia nchi zao na kujaribu kutatua migogoro iliyoko Duniani ili kila Nchi ipate Ustawi unaokusudiwa na Mungu.
Yeye aliye na sikio na alisikie neno hili ambalo Roho aliambia kanisa.
Rev. Innocent Kamote
Mkuu wa wajenzi Mwenye Hekima

Msichoke katika kutenda Mema!

Wagalatia 6:9Tena tusichoke katika kutenda mema; maana tutavuna kwa wakati wake, tusipozimia roho.


 Utangulizi:

Msichoke katika kutenda mema, Mstari huu katika biblia ya kiingereza unasomeka “And let us not grow weary while doing good, for in due season we shall reap if we do not lose heart”
Neno

“weary”
linalotumika hapo halizungumzii kuchoka kwa mwili ambako kunaweza kukarabatiwa kwa kula, kunywa maji mengi, kuoga maji ya baridi na kupumzika vya kutosha ambako kitaalamu kunaweza kuwa tiba ya kuchoka kwa mwili, Neno hili Weary maana yake spiritless, Exhausted, lose heart, despair hii inazungumzia kuchoka kwa nafsi huku ndio kuchoka kubaya zaidi kunakoweza kuleta madhara makubwa
Kuchoka huku ni hali ya kukata tamaa, ni hali ya kutokuendelea au hali ya kuvunjika moyo, Hali hii inatokana na kukosekana kwa muamko wa Moyo na sio kuchoka kwa mwili, Hali ya kukosa muamko inaweza kupelekea mtu kuchoka katika nafsi mwili na roho. Hivi karibuni watu tumeshuhudia huko Africa ya kusini watu waliochoka nafsi waliweza kuwavamia waafrika wenzao na kuharibu vitu na kuiba na kuchoma moto matendo ambayo yameleta aibu duniani lakini sababu kubwa inatokana watu kukata tamaa, watu wanapokata tamaa huweza kucha kutenda mema na wakatenda mabaya!

 Maandiko yanatuonya kutokukata tamaa kutokuchoka, kuchoka kunaweza kuletwa na Maswala mbalimbali makubwa katika maisha yetu, Nyakati za Kanisa la kwanza wakati mwingine Makanisa yalikata tamaa kutokana na kukamatwa kwa viongozi na kuwekwa ndani mara kwa mara Waefeso 3:13 “Basi naomba msikate tamaa kwa sababu ya dhiki zangu kwa ajili yenu, zilizo utukufu kwenu.” Watu wanapokosa mwamko ni rahisi sana kukata tamaa, wanafunzi wanapokosa mwamko ni rahisi kuchoka katika kusoma, walimu wanapokata tamaa ni rahisi sana kuendelea kuwafundisha wanafunzi kwa weledi, Baba anapochoka  anapochoshwa na tabia za watoto au mkewe  nyumbani anaweza kukata tamaa, kila tunalilofanya linahitaji motosha ili tusiweze kuchoka.

Msichoke Katika kutenda Mema.

Msichoke katika kutenda mema, hili ni swala ambalo neno la Mungu linatutia moyo, kwamba tuendelee kutenda mema kwa imani, kwa upendo, na nguvu tuliyonayo katika jina la Yesu, hii ni kanuni ambayo ina mavuno ndani yake , lakini sio hivyo tu ni jambo lenye kumpendeza Mungu; Hatupaswi kuchoka hata kidogo Mungu azitie moyo roho zetu na nia zetu, Hata tunapokutana na vikwazo vya namna mbalimbali, Mara nyingi ni vigumu kupata muelekeo na kuchoka kwa nafsi, Mabadiliko mbalimbali ya kiuchumi, Madeni, kupoteza maswala kadhaa katika ulimwengu, kukosekana kwa shukurani au kupongezwa au hata kutiwa Moyo ulimwengu unapokuwa sio ulimwengu wenye kutia moyo ni rahisi sana watu kukata tamaa na kuacha kufanya kile wanachojisikia kukifanya na hapo Biblia inatusukuma kutokuacha au kuchoka katika kutenda mema 2Wathesalonike 3:13 “Lakini ninyi, ndugu, msikate tamaa katika kutenda mema.”

Kunapotokea Maswala magumu ya kukatisha tamaa na kukosekana kwa motisha miongoni mwa wakristo ni rahisi sana kwa jamii ya kanisa kuacha kuendelea kutumika katika kiwango kile tulichokuwa nacho, ni rahisi kutoa udhuru, ni rahisi kupoteza mwelekeo na ni rahisi kuacha hii inatokana na kukata tamaa Tunahitaji neema ya Mungu na kutokukata tamaa kabisa Yakobo 5:7-8 “Kwa hiyo ndugu, vumilieni, hata kuja kwake Bwana. Tazama, mkulima hungoja mazao ya nchi yaliyo ya thamani, huvumilia kwa ajili yake hata yatakapopata mvua ya kwanza na ya mwisho. Nanyi vumilieni, mthibitishe mioyo yenu, kwa maana kuja kwake Bwana kunakaribia

 Neno la Mungu linatutia moyo kuwa Kutenda mema kunalipa na kuwa tutavuna kwa wakati, aidha wakati huu wa sasa ama wakati ujao liko tumaini kubwa mbele yetu na kamwe hatupaswi kuzimia moyo uvumilivu wetu unapaswa kuwa sawa na ule wa mkulima Mungu atatulipa tu kwani kila tulifanyalo lililo jema ni mbegu kwa MUngu na kwa wakati wake tutavuna kama hatutazimia moyo

Mfano:

Katika mji mmoja kulikuwa na vijana wawili waliokuwa Ndugu, Ndugu mkubwa alimuonea sana na kumtendea vibaya ndugu yake mdogo na wala hakuwahi kumuonyesha upendo, na wakati mwingine alikula chakula chake, na pia alichukua nguo zote nzuri za ndugu yake mdogo na kuzivaa yeye, Nduguye aliendelea kuvumilia na kumuonyesha upendo hatahivyo, Siku moja Ndugu yule mkubwa alikwenda msituni kwa kusudi la kutafuta kuni na kuziuza, alipokuwa msituni akikata kuni, kutoka mti mmoja mpaka mti mwingine, alikutana na mti mmoja wa ajabu, na mti huu ulimwambia tafadhali sana usikate matawi kutoka kwangu na kama utafanya hivyo nitakupa peasi la dhahabu, Kijana yule mkubwa alikubali, Lakini hata hivyo mti ule wa ajabu ulimpa matunda machahe ya dhahabu,kwa uroho na uchungu na tamaa, aliamua kutisha ule mti kuwa ataukata!kama mti huu hautatoa peasi nyingi zaidi, Mti huu wa ajabu kwa namna iaisyoweza kuelezeka ulitoa miiba mingi sana na ikamchoma yule jama amwili mzima na akawa anagaa gaa kwaajili ya kujinasua kutoka katika kujitoa miiba ile

Ndugu yake mdogo alipoona kuwa jua linakuchwa alipata hofu na aliamua kumtafuta kaka yake, na alikwenda mpaka msituni na kumkuta akiwa katika hali ngumu sana na aliamua kumsaidia kwa upendo, na kumuondoa miiba yote mwilini alipomaliza kaka yake alitambua wazi kuwa mdogo wake alikuwa na upendo wa kweli, aliomba radhi,kwa jinsi alivyokuwa akimfanyia ubaya ndugu yake na alimuahidi kumtendea mema tangu siku ile , Mti ule wa ajabu uliona yote yaliyotendeka na ukaridhika na badilikola kaka mkubwa ukawapa wote mapeas ya dhahabu waliyohitaji, wote maisha yao yalibadilika na wakaishi maisha ya upendo

tunajifunza nini kutoka kwa ndugu yule mdogo angechoka kutenda mema aisngevuna kwa wakati muafaka  nay eye na kak ayake wasingeweza kuwa na maisha ya furaha na mafanikio

Rev. Innocent Kamote.

Mkuu wa Wajenzi mwenye Hekima!

Jumamosi, 3 Agosti 2019

Jicho kwa jicho na jino kwa jino!


Mathayo 5:38-41Mmesikia kwamba imenenwa, Jicho kwa jicho, na jino kwa jino; Lakini mimi nawaambia, Msishindane na mtu mwovu; lakini mtu akupigaye shavu la kuume, mgeuzie na la pili. Na mtu atakaye kukushitaki na kuitwaa kanzu yako, mwachie na joho pia. Na mtu atakayekulazimisha mwendo wa maili moja, nenda naye mbili.






Utangulizi:
Ni muhimu kufahamu kuwa usemi huu Jicho kwa jicho  na jino kwa jino una asili yake kutoka katika sheria  za ukaldayo zilizojulikana kama sheria za “Hammurabi”, lakini vilevile zinapatikana katika sheria ya Musa yaani agano la kale hususani katika kitabu cha Kutoka na kile kitabu cha Walawi, Zaidi ya yote Yesu aligusia juu ya hili katika hutuba yake ya mlimani katika agano jipya, Maana yake katika maandiko ikiwa ni rahisi tu “kuwa atendaye uovu anastahili kupata adhabu sawa sawa na kosa lake”
Ni muhimu kufahamu kuwa sheria ya Musa ilipotolewa ilikuwa imezingatia maeneo makubwa matatu yakiwemo ya Kidini, Kimaadili na kisiasa au kisheria yaani ninaweza kukuchanganulia sheria au Torati katika mazingira matatu yafuatayo:-
1.       Ceremonial law – Sheria za maswala ya kidini namna na jinsi impaswavyo mtu kumuabudu Mungu.
2.       Moral law – Sheria za uadilifu maswala ya mahusiano na kuishi kwa amani na watu wote.
3.       Civil law – Sheria za kimahakama na kifalme namana na jinsi serikali inavyoweza kuendeshwa.
Kwa msingi huo sheria au usemi huu wa Jicho kwa jicho na jino kwa jino, unaangulkia katika maswala ya kimahakama ambayo kimsingi yanaangukia katika swala la sheria za kiutawala Civil Law, mbele ya hakimu/jaji au mwamuzi kwa msingi huo usemi wa jicho kwa jicho na jino kwa jino  ni usemi wenye kuonyesha msisitizo au kuonya Mahakimu na majaji au waamuzi kuhukumu kwa haki, kutenda haki, wanapoamua kesi za watu na Yesu hakuwa na neno juu ya hili.

Wajibu wa Mahakama na sheria  zetu leo Duniani.
Ni muhimu kufahamu kuwa sheria hii ya kimahakama Yesu hakuiondoa Mathayo 5:17Msidhani ya kuwa nalikuja kuitangua torati au manabii la, sikuja kutangua, bali kutimiliza” Yesu anataka mahakama na sheria zetu duniani kuzingatia usawa katika kutoa haki, Kama ilivyoagizwa katika torati, na  yeye analikabidhi jukumu hili kwa mamlaka za  kila taifa na serikali na ufalme, hususani mahakama zake kwamba zinapaswa kuwapa watu haki zao, zina wajibu wa kutimiliza majukumu yao kwa mujibu wa sheria, lakini vilevile Mabunge kuhakikisha kuwa yanapitia sheria zote zilizopitwa na wakati na zisizotoa haki kwa upande mmoja, kuhakikisha kuwa haki inatendeka, huku kila mtu akistahili malipo kulinga na kile alichokifanya, haki inaposimama inastawisha taifa zima, Mithali 14:34Haki huinua Taifa ; Bali dhambi ni aibu ya watu wote” Ustawi wa jamii nzima unakuja pale tu haki inapotendeka, Mungu anataka haki itendeke, kadiri Dunia inavyoharibika ndivyo jinsi haki inavyozidi kuwa bidhaa adimu, Taifa lolote, familia yoyote na taasisi yoyote na ufalme wowote ambao hautendi haki, utaangushwa lakini Mungu hustawisha na kuinua taifa ambalo linatenda haki, kwa msingi huo kila jamii ina wajibu wa kujenga tabia na mwenendo wa kutenda haki, ili tuweze kubarikiwa na Mungu, Mungu hawezi kutubariki wakati tukiwa tumejaa udhalimu au taifa lililojaa dhuluma.Aidha watu hukosa amani na furaha wanapotawaliwa na watu waovu au watu wasiosimamia haki na usawa Mithali 29:2Wenye haki wakiwa na amri watu hufurahi, Bali mwovu atawalapo watu huugua” Furaha na amani ya kweli katika jamii inapatikana kwa utawala wa haki, wenye kuhukumu kwa haki na kumuacha muovu awajibike kwa kile alichokifanya, Huu ndio mpango wa Mungu.

Kwa msingi huu Kanuni ya kutenda haki kwa mujibu wa Yesu kwa upande wa utawala inabaki vile vile katika kuhakikisha mahakama, wanasheria na Majaji na waamuzi wanatenda haki, wakiongozwa na kanuni, na sheria za jamii husika, huku sheria hii kutoka katika torati ya Musa ikiwa ndio msingi wa swala hili, wao wana wajibu wa kuwapatia watu haki zao, na kila jamii inapaswa kufanya hivyo hii ndio maana ya usemi wa Jicho kwa jicho na jino kwa jino.

Wajibu wa wanafunzi wa Yesu!
Baada ya Yesu kukamilisha fundisho juu ya umuhimu wa haki, ni muhimu kufahamu kuwa Yesu hakuondoa umuhimu wa kudai haki inayostahili, haki inapaswa kusimama vilevile kama ipaswavyo, watendao maovu wanapaswa kulipia uovu wao,lakini hili ni jukumu la kiutawala

Warumi 13:1-5 “Kila mtu na aitii mamlaka iliyo kuu; kwa maana hakuna mamlaka isiyotoka kwa Mungu; na ile iliyopo umeamriwa na Mungu. Hivyo amwasiye mwenye mamlaka hushindana na agizo la Mungu; nao washindanao watajipatia hukumu. Kwa maana watawalao hawatishi watu kwa sababu ya matendo mema, bali kwa sababu ya matendo mabaya. Basi, wataka usimwogope mwenye mamlaka? Fanya mema, nawe utapata sifa kwake; kwa kuwa yeye ni mtumishi wa Mungu kwako kwa ajili ya mema. Lakini ufanyapo mabaya, ogopa; kwa maana hauchukui upanga bure; kwa kuwa ni mtumishi wa Mungu, amlipizaye kisasi mtenda mabaya kwa ajili ya ghadhabu. Kwa hiyo ni lazima kutii, si kwa sababu ya ile ghadhabu tu, ila na kwa sababu ya dhamiri.
Kwa kuwa serikali zipo basi kila atendaye uovu anapaswa kulipwa sawa na haki za kisheria zilizoko katika utawala husika, Lakini wanafunzi wa Yesu kwa mujibu wa Mafundisho yake wanapaswa kuwa na uadilifu na kwenda mbali zaidi kuliko sheria inavyotaka ili mwenendo wao uweze kuwahubiri waovu wajue kuwa yuko Mungu, kwa hivyo kwa kupitia upendo wana wanapaswa kuwapenda adui zao, kuwa na utayari hata wa kuwasamehe  na kupoteza haki zao za kisheria na kuwalipa mema badala ya mabaya, Yesu anawataka wanafunzi wake kutokuitikia jambo lolote ovu katika namna ya chuki au kulipa baya kwa baya Mungu anataka tuushinde ubaya kwa wema

Warumi 12:17-21.Msimlipe mtu ovu kwa ovu. Angalieni yaliyo mema machoni pa watu wote. Kama yamkini, kwa upande wenu, mkae katika amani na watu wote. Wapenzi, msijilipize kisasi, bali ipisheni ghadhabu ya Mungu; maana imeandikwa, Kisasi ni juu yangu mimi; mimi nitalipa, anena Bwana. Lakini, Adui yako akiwa na njaa, mlishe; akiwa na kiu, mnyweshe; maana ufanyapo hivyo, utampalia makaa ya moto kichwani pake. Usishindwe na ubaya, bali uushinde ubaya kwa wema.”,

Yesu katika mafundisho yake anataka Wakristo tuonyeshe muitikio wenye uadilifu unaoonyesha kuwa sisi ni wanafunzi wa Yesu ili kupitia wema wetu walio gizani waweze kuiona Nuru, jambo hili ndilo linaloleta thawabu kwa Mungu, yaani watu wanapotukusudia mabaya sisi tuwakusudie mema tu

Mwanzo 50:19-21 “Yusufu akawaambia, Msiogope, je! Mimi ni badala ya Mungu? Nanyi kweli mlinikusudia mabaya, bali Mungu aliyakusudia kuwa mema, ili itokee kuokoa taifa kubwa, kama ilivyo leo. Basi sasa msiogope; mimi nitawalisha na watoto wenu. Akawafariji, na kusema nao vema.”
Yusufu alichukiwa bure tu na ndugu zake na tena walikusudia kumuua 

Mwanzo 37:18 “ Wakamwona  toka mbali na kabla hajawakaribia, wakafanya shauri juu yake ili wamuue”
kabisa na baadaye waliamua kumuuza utumwani, angeweza Yusufu kujilipizia kisasi lakini alionyesha mwitikio mwema alisema nao vizuri na aliwalisha wana na watoto zao ili Nduguze waweze kuuona wema wa Mungu katika uovu wao, Hiki ndicho Yesu alichokuwa amekikusudia katika neno lake, Yesu anawataka wakristo wavumilie na hatimaye wamuachie Mungu awalipizie Kisasi dhidi ya wale wote wanaotaka kuangamiza maisha yetu Bwana ataamua yeye mwenyewe lakini mkono wako usiwe juu ya adui yako anayekutafuta na Mungu atafanya tu 1Samuel 24:1-22, “Ikawa, Sauli aliporudi baada ya kuwafuatia Wafilisti, aliambiwa ya kwamba, Daudi yuko katika nyika ya Engedi. Ndipo Sauli akatwaa watu elfu waliochaguliwa katika Israeli wote, akaenda kumtafuta Daudi na watu wake juu ya majabali ya mbuzi-mwitu. Akafika penye mazizi ya kondoo kando ya njia, na huko kulikuwa na pango; Sauli akaingia ndani ili kuifunika miguu. Na Daudi na watu wake walikuwa wakikaa mle pangoni ndani sana. Nao watu wa Daudi wakamwambia, Tazama, hii ndiyo siku ile aliyokuambia Bwana, Angalia, nitamtia adui yako mikononi mwako, nawe utamtenda yo yote utakayoona kuwa mema. Basi Daudi akainuka, akaukata upindo wa vazi lake Sauli kwa siri. Lakini halafu, moyo wake Daudi ukamchoma, kwa sababu amekata upindo wa vazi lake Sauli. Akawaambia watu wake, Hasha! Nisimtendee bwana wangu, masihi wa BWANA,neon hili,kuunyosha mkono wangu juu yake,kwa maana yeye ni masihi wa BWANA. Basi Daudi akawazuia watu wake kwa maneno hayo, asiwaache kumwondokea Sauli. Kisha Sauli akatoka pangoni, akaenda zake. Daudi naye akainuka baadaye, akatoka pangoni, akamwita Sauli, akisema, Bwana wangu, mfalme. Na Sauli alipotazama nyuma, Daudi akainama uso wake hata nchi, akamsujudia. Daudi akamwambia Sauli, Kwa nini unasikiliza maneno ya watu wasemao, Tazama, Daudi anataka kukudhuru? Tazama, leo hivi macho yako yameona jinsi Bwana alivyokutia mikononi mwangu pangoni, na watu wengine wakaniambia nikuue; lakini nikakuacha; nikasema, Sitaki kuunyosha mkono wangu juu ya bwana wangu; kwa maana yeye ni masihi wa BWANA.Tena, baba yangu, tazama, tafadhali, tazama upindo wa vazi lako mkononi mwangu; maana ikiwa nimeukata upindo wa vazi lako, nisikuue, ujue, na kuona ya kuwa hakuna uovu wala kosa mkononi mwangu, wala sikukukosa neno; ingawa wewe unaniwinda roho yangu ili kuikamata. Bwana atuamue, mimi na wewe, na Bwana anilipizie kisasi changu kwako; lakini mkono wangu hautakuwa juu yako. Kama vile walivyosema watu wa kale katika mithali yao, Katika waovu hutoka uovu; ila mkono wangu hautakuwa juu yako. Na mfalme wa Israeli ametoka ili kumfuatia nani? Unamwinda nani? Ni kuwinda mbwa mfu, au kiroboto. Basi Bwana atuamue, akatuhukumu mimi na wewe, akaone, akanitetee neno langu, akaniokoe na mkono wako. Ikawa, Daudi alipokwisha kumwambia Sauli maneno hayo Sauli alisema, Hii ndiyo sauti yako, Daudi, mwanangu? Naye Sauli akapaza sauti yake, akalia.  Akamwambia Daudi, Wewe u mwenye haki kuliko mimi; maana wewe umenitendea mema, nami nimekutenda mabaya. Nawe umeonyesha leo jinsi ulivyonitendea mema, kwani Bwana aliponitia mikononi mwako, hukuniua.Maana mtu akimwona adui yake, je! Atamwacha aende zake salama? Basi Bwana na akulipe mema kwa haya uliyonitendea leo.  Na sasa, angalia, najua ya kuwa hakika utakuwa mfalme, na ufalme wa Israeli utafanyika imara mkononi mwako. Basi sasa, uniapie kwa Bwana, ya kwamba hutawakatilia mbali wazao wangu baada yangu, wala hutaliharibu jina langu katika mbari ya baba yangu. Naye Daudi akamwapia Sauli. Kisha Sauli akaenda zake kwao; lakini Daudi na watu wake wakapanda kwenda ngomeni.”
Unaweza kuona kwa msingi wa mafundisho hayo Yesu alikuwa anataka tuachilie haki zetu kwa kuutanguliza upendo hata kwa wale ambao ni adui zetu na sio hivyo tu hata kuwaombea, hii haina maana kuwa Mungu hataingilia kati hapana Mungu atawalipa wale wanaotutendea uovu watavuna kila walichokipanda kama hawatatubu na kubadilika kupitia wema wetu, kwa kuwa  Mungu hadhiahakiwi, Yesu alitaka tusishindane na mtu muovu, tusikae katika kanuni ya jicho kwa jicho au jino kwa jino alitaka tuonyeshe upendo wa Mungu kwa adui zetu ili waweze kujutia maovu yao kama ilivyotokea kwa Sauli na ndugu za Yusufu. Walitenda dhambi walikusudia mabaya Lakini Daudi na Yusufu walikusudia mema.

Warumi 12:20 “Lakini adui yako akiwa na njaa mlishe na akiwa na kiu mnyweshe, maana ufanyapo hivyo utampalia makaa ya moto kichwani
Mungu kwa neema yake na kwa wakati wake atalipa kisasi, kisasi ni juu yake Lakini sio hivyo tu tunaporejesha mema kwa waliotutenda uovu meama yatakaa katika nyumba zetu yaani ukoo wetu wote utabarikiwa lakini tukirejesha mabaya badala ya mema mabaya hayataondoka katika nyumba yetu yaani ukoo wetu

Mithali 17:13 “Yeye arudishaye mabaya badala ya mema, Mabaya hayataondoka nyumbani mwake.”
Kwa msingi huo kuba baraka kubwa sana mbele za Mungu na Mbele za Bwana wetu Yesu Kristo katika kulitendea kazi lile alilotuagiza  Yohana 13:17 “Mkiyajua hayo, heri ninyi mkiyatenda.”
Mkiyajua hayo heri ninyi mkiyatenda!
Rev. Innocent Kamote
Mkuu wa Wajenzi mwenye Hekima!