Ijumaa, 14 Februari 2020

Mtendeeni Yule Kijana Absalom kwa Upole kwaajili yangu!



2 SAMUEL 18:1-5Kisha Daudi akawahesabu watu waliokuwa pamoja naye, akaweka maakida wa elfu elfu, na maakida wa mia mia juu yao. Daudi akawapeleka hao watu vitani, theluthi moja chini ya mkono wa Yoabu, na theluthi ya pili chini ya mkono wa Abishai, mwana wa Seruya nduguye Yoabu, na theluthi ya tatu chini ya mkono wa Itai, Mgiti. Mfalme akawaambia watu, Bila shaka mimi mwenyewe nami nitatoka pamoja nanyi. Lakini watu wakasema, Wewe usitoke nje; kwa maana tukikimbia, hawatatuona sisi kuwa kitu; au tukifa nusu yetu, hawatatuona kuwa kitu; lakini wewe u wa thamani kuliko watu elfu kumi katika sisi; kwa hivyo sasa ni afadhali ukae tayari kutusaidia toka mjini. Mfalme akawaambia, Yaliyo mema machoni penu ndiyo nitakayofanya. Basi mfalme akasimama kando ya lango, na hao watu wakatoka kwa elfu zao na mia zao. Mfalme akawaamuru Yoabu na Abishai na Itai, akasema, Mtendeeni yule kijana, Absalomu, kwa upole kwa ajili yangu. Nao watu wote wakasikia, mfalme alipowaagiza maakida wote katika habari za Absalomu.”   

    

Utangulizi:-
Moja ya maswala magumu sana katika maisha ni pamoja na kufanya maamuzi hususani wakati mtu unayempenda na kumthamini anapokufanyia jambo baya sana na jambo hilo ukawa umelithibitisha, kuwa ni la kweli katika nyakati kama hizo.
·         Watu wengi huweza kutoa adhabu kali sana za kukomesha na kuangamiza pale wanapokuwa wamefanyiwa mambo mabaya.
·         Tumeshuhudia watu wakiwachoma moto watoto wadogo kwa sababu tu wamechukua fedha ua wameiba
·         Wengine wamewaadhibu kwa kuwachapa vibaya kwa mikanda na kuwajeruhi wakosaji
·         Wengine wamemwagiwa tindi kali, au kuwapeleka polisi
·         Wengine wamepeleka taarifa katika vyombo vya habari na magazeti
Makanisani pia tunashuhudia watu wakitengwa na kufukuzwa utumishi bila malipo yoyote, wakinyimwa posho, kutengwa miezi kadhaa, kufungiwa huduma kuchafuliwa na kuwazuia kihuduma ili yamkini ikiwezekana wasiinuke tena. Na kila wakati kunukuu taarifa zao kana kwamba wao ndio watu waovu zaidi wa kutolewa mifano
Je unafanya nini wakati uwapendao, watoto, ndugu, jamaa, rafiki, na kadhalika wanapokuasi na kusimama kinyume nasi na kuanza kutubomoa, wale tuliowagharimia wanapotukosea tunafanya nini?

2 Samuel 18:1-5
Katika kifungu hiki Daudi analazimika kupigana vita, vita hii ni mbaya kuliko zote alizowahi kupigana katika maisha yake ni vita ngumu safari hii mfalme hapigani na wafilisti wala Goliath wala maadui za Bwana anapigana na ndugu zake mwenyewe Israel wakiongozwa na mwanaye mwenyewe kijana wake mzuri aliyeitwa Absalom!
Hakuna vita mbaya duniani kama vita vya wenyewe kwa wenyewe, ni vita ngumu, ukisema ummalize adui ni kama unajimaliza mwenyewe

Mathayo 12:25-26 “Basi Yesu akijua mawazo yao, akawaambia, Kila ufalme ukifitinika juu ya nafsi yake, hufanyika ukiwa; tena mji au nyumba yo yote ikifitinika juu ya nafsi yake, haitasimama.  Na Shetani akimtoa Shetani, amefitinika juu ya nafsi yake; basi ufalme wake utasimamaje?”            
 

Yesu anaonyesha ubaya wa vita vya wenyewe kwa wenyewe vita hii ndio iliyokuwa ikimkabili Daudi wakati huu, hapa ilikuwa vita inayoweza kuleta ukiwa mkubwa sana na huzuni kubwa mno.
Vita yoyote ya Taifa kwa taifa yaani taifa lililogawanyika
Vita yoyote ya Familia iliyogawanyika
Vita yoyote ya mtu na mkewe au mtu na mumewe
Vita vya mtu na rafiki yake
Vita ya mtu na mchumba wake
Vita ya watoto na wazazi
Vita vya mtu uliyengharimia
Vita vya mchungaji na wachungaji wenzake au na wazee wa kanisa ama na washirika, vita vya taasisi moja inayofanana, vita vya wakristo kwa wakristo,
Au wanakwaya kwa wanakwaya

Vita za namna hii zinakuwa mbaya sana na zinasababisha ukiwa mkubwa hasa inapotokea kuwa upande mmoja unakusudia kuumlaliza upande mwingine kabisa huku hakuna anayefaidika na vita hiyo.
Haya ndiyo yaliyomkuta Daudi mara hii anapigana vita na mwanaye mpendwa mzuri aliyeitwa Absalom.
Absalom alikuwa kijana wa mfalme aliyesifiwa sana, alikuwa mzuri na msafi, alipendeza na kuvutia  na alikuwa na ushawishi kwa watu, alikuwa na nywele nzuri na ndefu ambazo zlilikatwa mara tatu tu kwa mwaka, hakuwa na ila ya aina yoyote kwa habari ya uzuri, pia alikuwa na akili hata hivyo mambo kadhaa yalichangia kuharibu maisha ya kijana huyu.
Alikuwa na Uchungu
 Alikuwa ni kisasi
Alikuwa na Hila
Alikuwa na kiburi na mwenye kukosa Subira pia hakuwa na msamaha

Mambo haya yalipelekea kijana huyu kumuasi baba yake na kujitangaza kuwa Mfalme 2Samuel 14:25-26”Basi katika Israeli wote hapakuwa na mtu hata mmoja mwenye kusifiwa kwa uzuri wake kama huyo Absalomu; tangu nyayo za miguu yake hata utosi wa kichwa chake hapakuwa na ila kwake. Naye aliponyoa kichwa, (basi mwisho wa kila mwaka hunyoa; na kwa sababu nywele zilikuwa nzito kwake, kwa hiyo akanyoa;) hupima nywele za kichwa chake shekeli mia mbili kwa uzani wa mfalme.”  

        
Kijana huyu alikuwa na uwezo wa kutumia hila na akili aliyonayo aliweza kuhadaa mioyo ya watu kwa muda wa miaka kama minne hivi 2Samuel 15:1-12, “Ikawa baada ya hayo, Absalomu akajiwekea tayari gari na farasi, na watu hamsini wa kupiga mbio mbele yake. Tena Absalomu huondoka asubuhi na mapema, na kusimama kando ya njia ya lango; kisha ikawa, mtu ye yote aliyekuwa na neno, lililokuwa halina budi kufika kwa mfalme ili kuhukumiwa, Absalomu humwita mtu huyo kwake, na kumwuliza, Wewe u mtu wa mji gani? Naye akasema, Mtumwa wako ni mtu wa kabila fulani ya Israeli.  Naye Absalomu humwambia, Tazama, maneno yako ni mema yenye haki; lakini hapana mtu aliyeagizwa na mfalme kukusikiliza. Tena Absalomu husema, Laiti mimi ningewekwa kuwa mwamuzi katika nchi hii, ili kila mtu mwenye neno au daawa aje kwangu, nimpatie haki yake! Tena ikawa hapo alipokaribia mtu ye yote kumsujudia, hunyosha mkono wake, na kumshika, na kumbusu. Hivyo ndivyo Absalomu alivyowatendea Israeli wote, waliomwendea mfalme ili wapate hukumu; na hivyo Absalomu akawadanganya watu wa Israeli. Hata ikawa mwisho wa miaka minne, Absalomu akamwambia mfalme Tafadhali uniache niende nikaondoe nadhiri yangu, niliyomwekea Bwana huko Hebroni. Maana mimi mtumishi wako naliweka nadhiri hapo nilipokuwa nikikaa Geshuri katika Shamu, nikasema, Kama Bwana akinirudisha Yerusalemu kweli, ndipo nitamtumikia Bwana. Naye mfalme akamwambia, Enenda na amani. Basi akaondoka, akaenda Hebroni. Lakini Absalomu akapeleka wapelelezi katika kabila zote za Israeli kusema, Mara mtakaposikia sauti ya tarumbeta, ndipo mtakaposema Absalomu anamilikl huko Hebroni. Na watu mia mbili walioalikwa wakatoka Yerusalemu pamoja na Absalomu, wakaenda katika ujinga wao wasijue neno lo lote. Absalomu naye akatuma kumwita Ahithofeli Mgiloni, mshauri wake Daudi, kutoka katika mji wake, yaani, Gilo, alipokuwa akitoa dhabihu. Fitina yao ikawa na nguvu; maana watu waliokuwa pamoja na Absalomu wakazidi kuwa wengi. 

Safari hii uasi wake ulikuwa na nguvu ya kupita kawaida na alitaka kuithibitishia Isarael ya kuwa kweli amaemuasi baba yake

2Samuel 16:21-23Naye Ahithofeli akamwambia Absalomu, Ingia wewe kwa masuria ya baba yako, hao aliowaacha ili kutunza nyumba; na Israeli wote watasikia ya kuwa umechukizwa kabisa na baba yako; ndipo itatiwa nguvu mikono yao wote walio pamoja nawe. Basi wakamtandikia Absalomu hema juu ya nyumba darini; naye Absalomu akaingia kwa masuria ya babaye machoni pa Israeli wote. Na shauri lake Ahithofeli, alilokuwa akilitoa siku zile, lilikuwa kama mtu aulizapo kwa neno la Mungu; ndivyo yalivyokuwa mashauri yote ya Ahithofeli, kwa Daudi, na kwa Absalomu.” 

   
Mshauri wa Absalom alishauri kuwa anayepaswa kuuawa hapa ni Daudi peke yake na sio vinginevyo ili watu wakae katika amani 2Samuel 17:1-4 “Zaidi ya hayo Ahithofeli akamwambia Absalomu, Niache nichague watu kumi na mbili elfu, nami nitaondoka na kumfuatia Daudi usiku huu; nami nitamshambulia wakati atakaokuwa amechoka, na mikono yake imekuwa dhaifu, nami nitamtia hofu; na watu wote walio pamoja naye watakimbia; nami nitampiga mfalme peke yake; na hao watu wote nitawarejeza kwako; mtu yule umtafutaye ni kana kwamba wamerudi wote; na hivyo watu wote watakuwa katika amani. Shauri hili likawa jema machoni pa Absalomu, na machoni pa wazee wote wa Israeli.” 

  
Unaweza kuona kuwa kijana wako uliyemzaa mwenyewe na ni Mashuhuri anakuasi waziwazi na anakusudia kukumaliza kabisa, amekuvunjia heshima yako hadharani amekudhalilisha anakuweka katika wakati mgumu je? katika hali kama hii unafanya nini hivi ndivyo Daudi alivyofanya nasi ni muhimu tukafanya au kujifunza kutoka kwake!

1.       Kubali kushuka

Watu wengi sana hususani vijana  na viongozi mbalimbali watu wao wanapowaasi, hawakubali kujishusha hata siku moja, wanataka kushughulikia matatizo wakiwa katika mamlaka yao ileile au katika mfumo wa cheo chao hujui mi mumeo, hujui mi askofu wako, Daudi alijua kuwa nia hii sio rahisi kufanikiwa kumpata mpendwa wake yeye aliamua kujishusha, aliachia ikulu na kukimbia pekupeku alijua kuwa hawezi kujiokoa wala kuwaokoa watu wake na mwanaye kama atabakia ikulu aliondoka

2samuel 15:14,30  Basi Daudi akawaambia watumishi wake wote waliokuwa pamoja naye Yerusalemu, Ondokeni, tukakimbie kwa kuwa tusipokimbia hapana mtu miongoni mwetu atakayeokoka mikononi mwa Absalomu; haya! Fanyeni haraka, tuondoke, asitupate Kwa upesi, Na kutuletea maovu, na kuupiga mji huu kwa makali ya upanga. , Daudi akapanda akishika njia ya kuupandia mlima wa Mizeituni, akilia alipokuwa akipanda; naye alikuwa amejifunika kichwa chake, akaenda hana viatu; na watu wote waliokuwa pamoja naye wakajifunika vichwa vyao, kila mmoja wao, wakapanda juu, wakilia walipopanda."            

Ili kumpata mwanadamu aliyeasi Yesu alikubali kuacha Enzi na utukufu, akanyenyekea kama mwanadamu mtumwa, watu wanavutiwa na mtu aliyejishusha, na sio Yule anayebaki ikulu, anayebaki katika haki yake na mamlaka yake, Absalom aliweza kuihadaa mioyo ya watu kwa sababu alijinyenyekeza kwao watu wakampenda

2Samuel 15:5-6,
Tena ikawa hapo alipokaribia mtu ye yote kumsujudia, hunyosha mkono wake, na kumshika, na kumbusu. Hivyo ndivyo Absalomu alivyowatendea Israeli wote, waliomwendea mfalme ili wapate hukumu; na hivyo Absalomu akawadanganya watu wa Israeli.         

Absalom alifahamu kuwa ili aipate mioyo ya watu  hana budi kujishusha katika kiwango chao, ili kuipata mioyo ya watu jishushe katika kiwango chao, Kamwe usitumie mamlaka yako katika kutatua matatizo, hujui mimi ni mzazi wako?, hujui mimi ni mumeo? Hajui mimi ndiye Rais?, hujui mimi ndiye Askofu? Atanitambua atajua kuwa mimi ndiye mwenyeji, mimi ndiye mwangalizi, mimi ndiye alwatani, mimi ndiye nimeshika mpini. Daudi aliacha viatu, alichukua namna ya mtumwa, aliondoka ikulu, Kujishusha kunasaidia kutatua matatizo,


1Samuel 25:5-8, Daudi akatuma vijana kumi, Daudi naye akawaambia hao vijana, Kweeni mwende Karmeli, na kumwendea huyu Nabali ili mnisalimie; na hivi ndivyo mtakavyomwambia huyu aishiye salama, Amani na iwe kwako, na amani nyumbani mwako, na amani kwao wote ulio nao. Nami sasa nimesikia ya kuwa una watu wanaokata manyoya kondoo zako; haya! Wachungaji wako wamekuwa pamoja nasi, wala hatukuwadhuru, wala hawakukosa kitu wakati wote walipokuwako huko Karmeli. Waulize vijana wako, nao watakuambia; basi na wakubaliwe vijana hawa machoni pako; maana tumekujia katika siku ya heri; uwape, nakusihi, cho chote kitakachokujia mkononi, uwape watumwa wako na mwanao Daudi.”
Unaona katikamkfungu hiki jinsi daudi anavyojishusha kwa Nabal wakati anaomba chakula?  Mungu humwangalia mtu mnyonge, mwenye roho iliyopondeka na kumuinua Isaya 66:2 “Maana mkono wangu ndio uliofanya hivi vyote, vitu hivi vyote vikapata kutokea, asema Bwana; lakini mtu huyu ndiye nitakayemwangalia, mtu aliye mnyonge, mwenye roho iliyopondeka, atetemekaye asikiapo neno langu.
Hatuwezi kutatua matatizo yetu bila kuamua kujishusha, kujishusha na roho ya unyenyekevu kumesaidia kujenga maisha ya watu wengi sana, kiongozi anayekaa ofisini tu bila kujali wala kujua matatizo ya watu na mahitaji yao, hawezi kukubaliaka na kufaa kwa Mungu na watu, Unyenyekevu ni njia ya kutupeleka juu sana katika kukubalika kwa Mungu na wanadamu tunapojishusha tunampa Mungu nafasi ya kuonyesha nguvu zake dhidi ya wale wanaotuandama kitendo cha Daudi kukimbia ikulu miguu peku na kulia na kurusha mavumbi juu kilikuwa ni kitendo cha kujishusha na kuhitaji neema ya Mungu kwamba Mungu aingilie kati katika mgopgoro huu mzito kati yake na mwanae mwenyewe, Yesu alikuwa ni Mungu na aliaxcha enzi na utukufu ili kuja duniani kutupatanisha tena isis tulioasi na kuturejesha mioyo yetu, Ndoa nyingi na migogoro mingi  duniani inawezankusuluhishwa kwa unyenyekevu endapo upande mmoja utajishusha!

2.       Rudisha sanduku la Mungu mahali pake 2Samuel 15:24-29

Na tazama, Sadoki naye akaja, na Walawi wote pamoja naye, huku wakilichukua sanduku la agano la Mungu; kisha wakalitua hilo sanduku la Mungu; Abiathari naye akapanda juu, hata watu wote walipokwisha kuutoka mji.  Naye mfalme akamwambia Sadoki, Rudisha sanduku la Mungu mjini; nikipata kibali machoni pa Bwana atanirudisha, na kunionyesha tena sanduku hili, na maskani yake;  lakini akisema kama hivi, Mimi si radhi nawe kabisa; basi, mimi hapa, na anitendee kama aonavyo kuwa vyema. Kisha mfalme akamwambia Sadoki, kuhani, Angalia, rudini mjini kwa amani, na wana wenu wawili pamoja nanyi, Ahimaasi,mwana wako, na Yonathani,mwana wa Abiathari. Angalia, mimi nitangoja penye vivuko vya jangwani, hata litakaponifikilia neno la kunipasha habari kutoka kwenu. Basi Sadoki na Abiathari wakalichukua sanduku la Mungu, wakalirudisha Yerusalemu; wakakaa huko. 

 
Sanduku la Agano la Mungu lilikuwa chombo muhimu sana chenye kuwakilisha uwepo wa Mungu, Ni chombo kinachoonekana kinachowakilisha uwepo wa Mungu asiyeonekana, Chombo hiki kilimwakilisha Yesu Kristo, aliye chapa ya mng’ao wa utukufu wa Mungu, Israel waliamini kuwa hata ukiingia vitani na chombo hiki lazima utashinda, Viongozi wengi sana wanapokuwa madarakani, huwa wanasahau kuwa unaweza kuwepo madarakani lakini Mungu au uwepo wa Mungu ukawa hauko pamoja nawe, unaweza kuwa mpakwa mafuta lakini Mungu akawa amekuacha, kama ilivyokuwa kwa Sauli mfalme, Ni lazima kwanza ufahamu Mungu yuko upande wa nani unapokuwa na migogoro, Absalom au wewe? Mungu yuko upande gani Hakuna mtu mwenye hati miliki ya uwepo wa Mungu, Mungu yuko kwaajili ya watu wote, si vema kuwahesabu wengine na kuwahukumu kama waasi tu, Daudi alitaka apate muda wa kupata na kusikia neno la Bwana ili kujua kuwa Bwana amempa kibali nani kati yake na Absalom, kama Bwana yuko na Absalom basi Absalom awe na uhuru wa kuabudu kupitia sanduku la agano, na kama Bwana yuko naye basi atampa neema ya kuliona sanduku hilo tena lakini sio kuondoka nalo, halikuwa la kwake lilikuwa kwaajili ya watu wote wa Mungu,

·         Viongozi wengi sana wa kiroho nimeona wakiwatenga watu wanaodhani kuwa ni wenye dhambi na zaidi ya yote huwafukuza na kuwanyima hata kuabudu, au kufanya huduma fulanifulani kabisa wakiwahesabia dhambi na kuwapimia muda wa miezi na hata miaka lakini huwa wanasahau kuwa kipimo cha utii katika moyo wa Mwanadamu anacho Mungu tu, Mtu hapimwi kwa kumzuia asihubiri, asiombe au asitoe sadaka huko ni kuhukumu na kujichukulia madaraka makubwa, wewe sio Mungu wala mimi sio Mungu huwezi kupima kati ya wewe na yule unayemdhania ni adui Mungu yuko na nani, huwezi kuwa na hati miliki ya uwepo wa Mungu, Mungu anaweza kuwa na yeyote tu Absalom au wewe, Daudi alifahamu hilo aliliacha sanduku la agano ili yeyeote anayetaka uwepo wa Mungu aukaribie.

·         Au wanaweza kumzuia mtu asifanyie wengine maombezi, swala la Ibada kwa binadamu liko wazi kwa kila mtu, swala la ibada halina hakimiliki, kuabudu ni swala huru kwa kila mtu hata kama sio wa dhehebu lako, Mungu si wa dehebu Fulani au dini Fulani kila mtu anahaki ya kuabudu na anapaswa kuabudu, kila mtu anapewa nafasi na maandiko na anapewa haki ya kuufikia uwepo wa Bwana Luka 9:49-50, Yohana akajibu akamwambia; Bwana mkubwa, tuliona mtu anatoa pepo kwa jina lako; tukamkataza, kwa sababu hafuatani na sisi. Yesu akamwambia, Msimkataze, kwa kuwa yeye ambaye si kinyume chenu yu upande wenu.” Matendo 4:18-20 “Wakawaita, wakawaamuru wasiseme kabisa wala kufundisha kwa jina la Yesu. Petro na Yohana wakawajibu wakawaambia, Kwamba ni haki mbele za Mungu kuwasikiliza ninyi kuliko Mungu, hukumuni ninyi wenyewe; maana sisi hatuwezi kuacha kuyanena mambo tuliyoyaona na kuyasikia.” Ni kwa kujua haya Daudi aliwaambia makuhani walirudishe sanduku la agano mahali pake, Mungu atusaidie kuwa na moyo kama wa Daudi wa kutambua kuwa uwepo wa Mungu sio hatimiliki ya mtu fulani, au kanisa Fulani au mchungaji Fulani au askofu Fulani kila mtu ana haki ya kuabudu.

3.       Fanya maombi ya kujidhili (Kujishusha).

2samuel 15:30-32 “Daudi akapanda akishika njia ya kuupandia mlima wa Mizeituni, akilia alipokuwa akipanda; naye alikuwa amejifunika kichwa chake, akaenda hana viatu; na watu wote waliokuwa pamoja naye wakajifunika vichwa vyao, kila mmoja wao, wakapanda juu, wakilia walipopanda.  Mtu mmoja akamwambia Daudi ya kwamba, Ahithofeli yu katika hao waliopatana na Absalomu; Daudi akasema, Ee Bwana, nakusihi, uligeuze shauri la Ahithofeli liwe ubatili. Ikawa, Daudi alipofika juu, hapo Mungu alipoabudiwa, tazama, Hushai, Mwarki, akaja kumlaki na joho lake limeraruliwa, tena ana udongo kichwani mwake.”
               
Daudi alifanya maombi ya kujidhili yaani alijishuhsa, alilia, hakwenda mbele za Mungu kama mwanamume na mfalme bali alikwenda kama mjakazi wa kike, alijifunika kichwa alipokuwa akimuomba Mungu

Kutoka 34:29-35, Hata ikawa, Musa aliposhuka katika mlima Sinai, na zile mbao mbili za ushuhuda zilikuwa mkononi mwa Musa, hapo aliposhuka katika mlima, Musa hakujua ya kuwa ngozi ya uso wake iling'aa kwa sababu amesema naye. Basi Haruni na wana wote wa Israeli walipomwona Musa, tazama, ngozi ya uso wake iling'aa; nao wakaogopa kumkaribia. Musa akawaita; Haruni na wakuu wote wa kusanyiko wakarudi kwake; Musa akasema nao. Baadaye wana wa Israeli wote wakakaribia; akawausia maneno yote ambayo BWANA amemwambia katika mlima Sinai. Na Musa alipokuwa amekwisha kusema nao, akatia utaji juu ya uso wake. Lakini desturi ya Musa ilikuwa alipoingia mbele za BWANA kusema naye, kuuvua huo utaji mpaka atoke; akatoka akawaambia wana wa Israeli maneno yote aliyoambiwa.  Wana wa Israeli wakauona uso wa Musa ya kuwa ngozi ya uso wake Musa iling'aa; naye Musa akautia utaji juu ya uso wake tena, hata alipoingia kusema naye.

 
Mwanamume hapaswi kufunika kichwa anapoingia katika uwepo wa Mungu, kuomba, hivyo maombi na dua za Daudi zilihusisha kujishusha kwa kiwango kikubwa na cha hali ya juu, Musa alipoingia katika uwepo wa Mungu kwa kusudi la kusema naye hakujifunika kichwa, alijifunika kichwa alipotoka, Mwanaume hapaswi kufunika kichwa chake anapokuwa katika uwepo wa Mungu ndiomaana wakristo huwa tunaondoa kofia wakati wa kusali  kwa desturi za kikristo ni aibu mwanaume kuingia katika uwepo wa Mungu akiwa amefunika kichwa chake angalia katika

 1Wakoritho 11:3-7, Lakini nataka mjue ya kuwa kichwa cha kila mwanamume ni Kristo, na kichwa cha mwanamke ni mwanamume, na kichwa cha Kristo ni Mungu. Kila mwanamume, asalipo, au anapohutubu, naye amefunikwa kichwa, yuaaibisha kichwa chake. Bali kila mwanamke asalipo, au anapohutubu, bila kufunika kichwa, yuaaibisha kichwa chake; kwa maana ni sawasawa na yule aliyenyolewa.  Maana mwanamke asipofunikwa na akatwe nywele. Au ikiwa ni aibu mwanamke kukatwa nywele zake au kunyolewa, na afunikwe.  Kwa maana kweli haimpasi mwanamume kufunikwa kichwa, kwa sababu yeye ni mfano na utukufu wa Mungu. Lakini mwanamke ni utukufu wa mwanamume.”        
Tendo la Daudi kumuomba Mungu huku amefunika kichwa kilikuwa ni kitendo cha kujishusha sana alijihesabu kama mjakazi wa kike mbele za Mungu aliweka mbali ufalme wake na uanaume wake na ujemedari wake alijidhili mnombele za Mungu na dua zake zilisikiwa

Luka 18:9-14
Akawaambia mfano huu watu waliojikinai ya kuwa wao ni wenye haki, wakiwadharau wengine wote.  Watu wawili walipanda kwenda hekaluni kusali, mmoja Farisayo, wa pili mtoza ushuru. Yule Farisayo akasimama akiomba hivi moyoni mwake; Ee Mungu, nakushukuru kwa kuwa mimi si kama watu wengine, wanyang'anyi, wadhalimu, wazinzi, wala kama huyu mtoza ushuru.  Mimi nafunga mara mbili kwa juma; hutoa zaka katika mapato yangu yote.  Lakini yule mtoza ushuru alisimama mbali, wala hakuthubutu hata kuinua macho yake mbinguni, bali alijipiga-piga kifua akisema, Ee Mungu, uniwie radhi mimi mwenye dhambi. Nawaambia, huyu alishuka kwenda nyumbani kwake amehesabiwa haki kuliko yule; kwa maana kila ajikwezaye atadhiliwa, naye ajidhiliye atakwezwa.Mungu hakubalia maombi ya watu wenye kujihesabia haki, Daudi alifahamu kuwa anahitaji maombi ya kujinyenyekesha wakati huu kupita kawaida ili hatimaye Mungu aweze kumuinua tena, alirusha michanga juu alitembea pekupeku alijifunika kichwa na kulia Mungu alisikiliza dua zake kutokana na unyenyekevu mkubwa alioonyesha mbele zake.

4.       Panga vita (Mikakati) ya ukombozi.

Ni muhimu kukumbuka kuwa hakuna vita ngumu duniani kama vita ya ndugu kwa ndugu, vita ya aina hii haina mshindi, ni ngumu na ni lazima  itaacha majeraha yanayoweza kudumu kwa muda mrefu, huwezi kupanga vita ya ndugu ikawa vita ya kumalizana, mwisho wa yote utalia mwenyewe, Ni lazima vita ya aina hii iwe vita ya ukombozi 2Samuel 18:1-5Kisha Daudi akawahesabu watu waliokuwa pamoja naye, akaweka maakida wa elfu elfu, na maakida wa mia mia juu yao. Daudi akawapeleka hao watu vitani, theluthi moja chini ya mkono wa Yoabu, na theluthi ya pili chini ya mkono wa Abishai, mwana wa Seruya nduguye Yoabu, na theluthi ya tatu chini ya mkono wa Itai, Mgiti. Mfalme akawaambia watu, Bila shaka mimi mwenyewe nami nitatoka pamoja nanyi. Lakini watu wakasema, Wewe usitoke nje; kwa maana tukikimbia, hawatatuona sisi kuwa kitu; au tukifa nusu yetu, hawatatuona kuwa kitu; lakini wewe u wa thamani kuliko watu elfu kumi katika sisi; kwa hivyo sasa ni afadhali ukae tayari kutusaidia toka mjini. Mfalme akawaambia, Yaliyo mema machoni penu ndiyo nitakayofanya. Basi mfalme akasimama kando ya lango, na hao watu wakatoka kwa elfu zao na mia zao. Mfalme akawaamuru Yoabu na Abishai na Itai, akasema, Mtendeeni yule kijana, Absalomu, kwa upole kwa ajili yangu. Nao watu wote wakasikia, mfalme alipowaagiza maakida wote katika habari za Absalomu. Daudi aliona uzito wa vita hii kwani sasa hapigani na Mfilisti wala Goliath anapigana na mwanaye aliyetoka katika viuno vyake.

Vita unayopigana na nduguyo ni lazima iwe vita ya ukombozi, Mara nyingi viongozi wengi wa kiroho na Kikristo, kunapotokea shida za kimahusiano mioyo yao hubadilika na kusahahu hili, mapambano yao na makusudi yao yanakuwa ni kumaliza kabisa au kumuumiza nduguyo, kumpoteza, kufuta jina lake kumfanya akome, asione suluhu tena Daudi hakutaka kabisa kumpoteza Absalom aliagiza wazi mbele ya makamanda wote “MTENDEENI YULE KIJANA ABSALOM KWA UPOLE KWAAJILI YANGU” haya ni maneno mazito Daudi aliyasema haya hadharani, na watu wote walisikia, alikuwa na moyo, Daudi alikuwa na moyo wa kiungu, siku zote Mungu anapotuadhibu kwaajili ya makosa yetu na dhambi hutuadhibu kwa kusudi la kuturekebisha na kuturejesha, na sio kutuangamiza, Daudi alitambua udhaifu wa mwanawe Absalom kuwa ni ujana ndio unaomsumbua ni mchanga ni kuwa hajakomaa hajajua maisha, ni dasari ndogondogo zinamsumbua na aliona ni afadhali angelikufa yeye badala ya mwanawe Asalom  hakuona ufahari kupoteza hata pamoja na kuwa amemwasi alitamani kuuona tena uso wa mwanae kipenzi


2Samuel 18:33-19:4  Naye mfalme akataabika sana, akapanda juu, akaingia kile chumba kilichokuwa juu ya lango, akalia; na katika kwenda kwake alisema hivi, Mwanangu Absalomu! Ee mwanangu! Mwanangu Absalomu! Laiti ningalikufa badala yako, Absalomu, mwanangu, mwanangu! - Mfalme akajifunika uso; na mfalme akalia kwa sauti kuu, Mwanangu Absalomu, Absalomu, mwanangu, mwanangu!” Biblia inasemaje ndugu yako anapokukosea ni lazima arejeshwe kwa upole Wagalatia 6:1Ndugu zangu, mtu akighafilika katika kosa lo lote, ninyi mlio wa Roho mrejezeni upya mtu kama huyo kwa roho ya upole, ukijiangalia nafsi yako usije ukajaribiwa wewe mwenyewe.”               

Daudi alikuwa na moyo wa urejeshi huu ndio moyo wa Mungu ndio moyo wa mtu aliyekomaa kiroho, awaye yote anayefurahia kuangamia na kupotea kwa ndugu yake na kumpoteza kabisa na akaona sawa sawa huyu atakuwa ana matatizo makubwa mno, Yuko tafauti na Moyo wa Mungu na wa Daudi.

Mungu kamwe hafurahii kufa kwake mtu mwenye dhambi Ezekiel 33:11 Waambie, Kama mimi niishivyo, asema Bwana MUNGU, sikufurahii kufa kwake mtu mwovu; bali aghairi mtu mwovu, na kuiacha njia yake mbaya, akaishi. Ghairini, ghairini, mkaache njia zenu mbaya; mbona mnataka kufa, Enyi nyumba ya Israeli?       
Daudi hakufurahia kifo cha Absalom mwanawe, ambaye kwa vyovyote alikuwa hajaifikilia toba, Upendo wa kweli haufurahii udhalimu, Moyo wa Daudi ulikuwa tayari, kufanya kitu kwaajili ya mtu muovu, kuliko watu wema waliokuwa upande wake 2Samuel 19:5-6Basi Yoabu akaingia nyumbani kwa mfalme, akasema, Wewe leo umefedhehesha nyuso za watumishi wako wote, waliokuokoa leo roho yako, na roho za wanao, na za binti zako, na roho za wakezo, na roho za masuria wako; KWA KUWA UNAWAPENDA WAKUCHUKIAO, NA UNAWACHUKIA WAKUPENDAO. Maana umetangaza leo ya kuwa wakuu na watumishi wako si kitu kwako; maana leo nimetambua hivi; kama Absalomu angaliishi, na sisi sote tungalikufa leo, ingalikuwa vyema machoni pako”.            

Ulikuwa ni moyo wa ajabu sana na upendo mwingi usioweza kupimika najua angekuwa mtu mwingine angesema ndio afadhali kafa, Mungu kamlipizia kisasi, Mungu ameshughulikia adui zangu lakini huu haukuwa moyo wa Daudi na sio moyo wa Mungu. Ni mara ngapi tumeweza kujishughulisha na watu wanaofikiriwa kuwa wamerudi nyuma, au mara ngapi tumewajali watumishi nwanaofikiriwa kuwa wameanguka na je tumejishughulisha vipi kuirejesha mioyo yao au je umehakikisha kuwa nduguyo amerejea katika toba? Wengi wetu mtu akianguka tunamuita muasi akihama dhehebu tunavunja urafiki naye tunadhani kuwa hastahili tena hafai huo sio moyo wa mtu anayeupendeza Moyo wa Mungu kama ilivyokuwa kwa Daudi tuna kitu cha kujifunza kwake

5.       Mtendeeni kwa Upole

Ingawa Absalom alikuwa amekusudia kumuua baba yake na kuwaacha watu hai, Daudi alikusudia wazi kwamba Absalom aachwe hai, Daudi alitoa nafasi ya pili kwa mkosaji, alitoa nafasi ya tatu na nne na tano na kuendelea, ni vema kuwapa wakosaji nafasi nyingine tena nani ajuae kuwa mioyo yao itabadilika nani ajuaye kuwa watakuwa wamejifunza maswala kadhaa? Naniajuaye kuwa makosa yao ilikuwa njia ya roho wa Mungu kuwafundisha kitu kama ilivyokuwa kwa mwana mpotevu? Je Mungu amemaliza kazi nao? Lazima tujihoji?

Daudi hakutaka kushindana na Absalom ni muhimu kufahamu kuwa hatupaswi kushindana na mtu aliye chini yako, Daudi hakuhesabu kuwa yuko vitani huwezi kupigana na mwanao hata kama yeye ni shetani, Mungu hapigani na shetani, hata siku moja ingawa yuko chini yake ni ujinga, Daudi hakufurahia kufa kwa mwanaye, hakufurahia kifo cha kudhalilika cha mwanaye ingawa yeye alikuwa amedhalilishwa na mwanaye, Daudi anaumia sana asiposamehe, alipenda kama angelipata nafasi ya kumtangazia mwanaye msamaha, alijuta kuikosa  nafasi hiyo alitamnani kama laiti angelipata nafasi ya kumwambia mwanangu nimekusamehe, Dhambi ya Absalom ni maumivu kwa Daudi Isaya 43:25 “Mimi, naam, mimi, ndimi niyafutaye makosa yako kwa ajili yangu mwenyewe, wala sitazikumbuka dhambi zako.”  Mungu anapotusamehe dhambi hutusamehe kwaajili yake mwenyewe upendo wake unamsukuma kusamehe na anaumia anapokosa nafasi ya kutusamehe anatamani tuhojiane naye anatamani tumjie tena ili azisafishe dhambi zetu anatamani kututendea kwa upole hataki mtu aangamie hafurahii mtu awaye yote apotee anataka watu wote wafikie toba 2Petro 3:9 “Bwana hakawii kuitimiza ahadi yake, kama wengine wanavyokudhani kukawia, bali huvumilia kwenu, maana hapendi mtu ye yote apotee, bali wote wafikilie toba.” , unaweza kuona Daudi anamtaka kijana Absalom aachiwe uhai wake asife na dhambi ni mwanae anampenda na aliagiza wazi  “Mtendeeni Yule kijana Absalom kwa upole kwaajili yangu” Tabia ya Daudi ni tabia ya uungu inayoonyesha ukomavu wa hali ya juu, wenye kujitoa usio na ubinafsi wenye kujali maisha ya wengine.

Daudi hakumuhukumu Absalom kwa vyovyote vile alimuachia Mungu ahukumu adui zake na wote waliomkataa na kumkana.

Mungu ndiye hakimu wa kweli atakayehukumu kwa haki dhidi nya maisha yetu
Mtazamo wako si ukweli kuhusu Mungu wakati wote.

Rev. Innocent Kamote
Mkuu wa wajenzi mwenye hekima!

Jumatatu, 10 Februari 2020

Chochea Karama ya Mungu iliyo ndani yako!

2Timotheo 1:3-6Namshukuru Mungu, nimwabuduye kwa dhamiri safi tangu zamani za wazee wangu, kama vile nikukumbukavyo wewe daima, katika kuomba kwangu usiku na mchana.  Nami natamani sana kukuona, nikiyakumbuka machozi yako, ili nijae furaha; nikiikumbuka imani uliyo nayo isiyo na unafiki, ambayo ilikaa kwanza katika bibi yako Loisi, na katika mama yako Eunike, nami nasadiki wewe nawe unayo. Kwa sababu hiyo nakukumbusha, uichochee karama ya Mungu, iliyo ndani yako kwa kuwekewa mikono yangu.”


Utangulizi:


Ni muhimu kufahamu kuwa kila mwanadamu amezaliwa kwa kukiwa na kusudi fulani au wajibu fulani wa kuutimiza ulioko ndani yake, na katika wajibu huo ili aweze kuutimiza ipaswavyo, Mungu huweka karama au kipawa kwaajili ya kumuwezesha mtu huyo kutimiza kusudi la Mungu lililowekwa ndani yake 


Hata hivyo karama au kipawa kinapokuwa ndani ya mtu kuna maswala kadhaa yanayopaswa kufanyika ili kiweze kukua au kukomaa au kujitokeza katika ubora wake swala hilo sio lingine ni kuchochea kipawa hicho kilichomo ndani ya mtu aliyekusudiwa na Mungu kutumiwa katika shughuli husika. Tutajifunza somo hili muhimu kwa kuzingatia vipengele vitatu vifuatavyo:-



·         Maana ya kuchochea Karama
·         Jinsi karama zinavyochochewa!
·         Namna karama zinavyochochewa!


Maana ya kuchochea Karama 

Paulo mtume anamwandikia Muhubiri na kiongozi kijana na mchanga katika Imani na maongozi ili kumtia moyo wakati yeye akiwa anaelekea ukingoni wakati huu Paulo mtume alikuwa gerezani kwa sababu ya injili, akisubiri kuuawa kwake muda si mrefu kwa hiyo anaandikwa waraka huu akiwa na hisia kali sana akijua ya kuwa anatengwa na wapendwa wake lakini vilevile akijua kuwa Timothy atakabiliwa namaswala mengi ya kuhubiri injili, uongozi, nausimamizi wa kanisa na shughuli nyingunezo katika jamii, na sasa anataka kumtia moyo ili asimame kiume awe imara ahakikisha anafanya kazi kwa bidii na uaminifu na ndipoi anaposema manenoi haya “Kwa sababu hiyo nakukumbusha uichochee karama ya Mungu, iliyo ndani kwa kuwekewa mikono yangu”Neno hili katika biblia ya kiingereza NKJV (New King James Version) linasomeka hivi “Therefore I remind you to stir up the gift of God which is in you trough the laying of my hands” Biblia  nyingine zimetumia neno “Keep a blaze the gift” na neno “rekindle the gift” Maneno ya kiyunani yanayotumika katika lugha hii ni “xesikono” yaani kuchochea mfano wa kusogeza vijinga vya moto ili moto wa kutumia kuni uweze kuendelea kuwaka, kwa kawaida moto wa kuni kama umewashwa na ukaachwa bila kuchochewa unaanza kuzimika na ili uendelee kuwaka vema unahitaji kuchochewa, Moto unapochochewa huwa na tabia ya kuendelea kuwaka na kubaki katika hali ileile na nguvu ileile au kuwaka zaidi.  Paulo anamtaka Timotheo aendelee kuwaka na kubaki katika hali ile ile na nguvu ileile au kuwaka zaidi, akiwa na imani ileile kama iliyokuwa kwa bibi yake loisi na mama yake Eunike nay eye mwenyewe aliwa kamawao na kuzidi. Kwa hiyo wale wanaotumia tafasiri ya kuchochea kwa maana ya kukoroga mfano wa sukari kwenye chai maana hjii ni ya kipuuzi kwa mujibu wa asili ya maandiko haya hayazungumzii kukoroga yanazungumzia kuongeza moto kuchochea kuhakikisha moto unabaki pale plale au unaendelea.


Hii ina maana gani? Matokeo makubwa katika jambo lolote tunalolifanya yatawezekana kama moto wetu hautazimika, Chakula kitaiva vizuri na Matunda yataonekana kama hakuna mtu anazimia moyo, Mungu amempa kila moja wetu karama na vipawa kwaajili ya shughuli mbali mbali, ili kufanikisha huduma na utumishi aliouweka ndani yetu na ndani ya kila mmoja wetu, Kama wewe ni mwana michezo mfano Bondia na umefanikiwa kuchukua mikanda mbalimbali ya kimataifa haupaswi kuishia hapo, Kama ni shule ya msingi au sekondari na imefanikiwa kiwilaya au kimkoa au kitafifa kushika nafasi nzuri ya juu kwa kufaulisha zaidi katika mitihani ya kitaifa haipaswi kuridhika na kubweteka na kukaa hapohapo tu, Kama ni kanisa limefanikiwa kuwahubiri injili watu maelefu kwa maelfu na kuwaleta kwaq Yesu hawapaswi kuridhika na kuishia hapohapo, kama Mungu amekupa nafasi ya kuwa Kiongozi mkubwa wanchi yaani Rais, au makamu wa Rais au waziri waziri mkuu, au  jaji mkuu au mkuu wa jeshi la pilisi, au Magereza, au uhamiaji, au zimamoto au kujenga taifa au mkuu wa majezi ya ulinzi na usalama,  spika wa bunge au mkuu wa mkoa au mbunge au mkuu wa wilaya na kadhalika na viongozi wengine wote na katika kanisa vilevile Hatupaswi kuishia hapo lazima tuichochee moto wa maendeleo na kuhakikisha kuwa kila tulifanyalo haliwi nguvu ya soda lazima tuchochee moto wa maendeleo na kuhakikisha kuwa tunasonga mbele na kupiga hatua kubwa sana hiki ndicho Mungu anachokitaka,  Mungu anataka moto uwe mkali zaidi, Nimeona pia katika nchji yetu Makocha wengi wa mpira wa miguu wanatoka katika nji nyingine kana kwamba hatuna makocha hodari hapa nyumbani Makocha wa nyumbani wanapaswa kuchochea uwezo wao na kujiapiza kuifunga kila timu yenye kocha mgeni mpaka wakubali kuwa nyumbani tunaweza hiki ndio kitu Mungu anataka, mpaka ulimwengu ugundue kuwa wako watu wanaweza, ikiwa wewe ni muhubiri hubiri injili kwa viwango na ufanisi mkubwa, ikiwa wewe ni mwanamuziki wa injili imba kwa mafundisho yaliyo sahihi huku wewe mwenyewe ukiwa ni kielelezo cha kila unachokihubiri, mwimbaji wa nyimbo za kawaida wekeza hisia zako zote kwa bidii, mchezaji wa mpira, bondia, mwanariadha, mwalimu, mwanafunzi, nakila mtu hata katika ndoa zetu hatuna budi kuhakikisha kuwa tunachochea upendo, uzalendo na mshikamano na kuhakikisha kuwa unawake na kuwa moto mkali sana na tutaona maendeleo makubwa katika taifa letu, Kila mmoja akichochea kipawa na karama aliyopewa na Mungu matunda yetu hayawezi kuzimika na kila sekta katika taifa letu itaonekana ikistawi kwa namna ya kipekee na ya tofauti, Na ndio maana Paulo mtume alikuwa anamtaka Timotheo aichochee karama ya Mungu iliyomo ndani yake, Leo mimi nawataka wananchi wote kwa pamoja tuchochee kila karama na kipawa kilichomo ndani yetu kila ambacho Mungu ametupa na kuwa tusizimie moyo wala tusiogope.

Paulo mtume alikuwa akimuomba Mungu na kutamani kuona Maisha ya Timotheo yanakwenda juu zaidi ya pale alipokuweko na kuwa imani yake inapaa na kuongezeka, Paulo alikuwa anajua kuwa Timotheo ana vipawa vingi na anajua kuwa zikichochewa atafanya na kuwa bora zaidi, Kila mtu na kila mmoja wetu ana kipawa fulani ndani yake na karama ambazo mungu ameweka ndani yetu kwa makusudi mbalimbali lakini hatuwezi kujigundua mpaka mtu mwingine aone, atuchochee na kututia moyo, Kila mwanadamu anahitaji kutiwa moyo, Hakuna mwanadamu anayefurahia kutukanwa kila siku na kukashifiwa na kuambiwa kuwa hana lolote, Ni lazima tuwe na tabia chanya yenye kuwajenga na kuwatia moyo wengine badala ya kuwa watu wenye kuonyesha kuwa wengine hawawezi ilihali kumbe ni sisi ndio hatuwezi, swala la kutia moyo mtu na kumuona mtu akifanya vema halihitaji kusomea saikolojia ni falsafa ya asili tu “Natural Philosophy” Mara kadhaa mtoto anapoanza kusimama katika mila na desturi zetu huwa tunawaimbia kamimama peke yake kwamakusudi la kuwatia moyo wasimame, kweli kweli  na hatimaye husimama, Wanamichezo wa soka na wa aina mbalimbali wanawahitaji sana washabiki wao kufika kwa wingi uwanjani ili kuwatia moyo na kuwashangilia jambo hili huwapa moyo na kuwafanya wafanye bidii na kufanikiwa, Mungu anapokuwa ameweka vipawa ndani yetu na karama za aina mbalimbali zinahitaji watu wenye ujuzi wa kututia moyo na kuhakikisha kuwa kwa namna chanya wanatujenga na kututia moyo ili kipawa na karama zisipotee na kufifia.


Jinsi Karama zinavyochochewa!


Ndani ya Timotheo kulikuwa na Huduma au karama ya Uongozi, yeye aliitwa na Mungu na kufanya kazi na Paulo mtume akisimamia makanisa alikuwa anapaswa kuyaongoza makanisa alikuwa nafanya kazi za kichungaji, alikuwa ni mwangalizi wa makanisa ya Mungu ni askofu kijana, alikuwa Muhubiri wa injili lakini kama binadamu alikuwa muoga kidogo, na alikuwa mwenye haiba ya aibu hivi na Paulo alifahamu jambo hili  na hivyo alitaka kumtia moyo asiogope kwani Mungu hakutupa roho ya woga ona 2Timotheo1:7Maana Mungu hakutupa roho ya woga, bali ya nguvu na ya upendo na ya moyo wa kiasi.” Hii maana yake ni kuwa Mungu anaweza kutupa vipawa vikubwa sana ndani yetu lakini kuna madhaifu ya kibinadamu inaweza kuwa woga, inaweza kuwa tunaona aibu au tunakosa nidhamu na kadhalika au tunaweza kuwa waoga na kwa kujua hili ndipo Mungu huwapa watu wake Roho Mtakatifu ili kuwawezesha kuwa wajasiri na kukabiliana na kila aina ya upinzani na kuweza kujihami dhidi ya upinzani wowote tutakaokutana nao Luka 12:11-12 “Na watakapowapeleka ninyi mbele ya masinagogi na maliwali na wenye mamlaka, msifadhaike kwa kuwaza maneno yenu jinsi mtakavyojibu au kusema; kwa kuwa Roho Mtakatifu atawafundisha saa ile ile yawapasayo kuyasema”. Matendo 1:8 “Lakini mtapokea nguvu, akiisha kuwajilia juu yenu Roho Mtakatifu; nanyi mtakuwa mashahidi wangu katika Yerusalemu, na katika Uyahudi wote, na Samaria, na hata mwisho wa nchi.” na Warumi 8;26 “Kadhalika Roho naye hutusaidia udhaifu wetu, kwa maana hatujui kuomba jinsi itupasavyo, lakini Roho mwenyewe hutuombea kwa kuugua kusikoweza kutamkwa.” Mungu yupo kututia nguvu na kutuwezesha na kutupa nidhamu na kiasi kuweza kushinda changamoto mbalimbali tunazokabiliana nazo katika maisha, Roho Mtakatifu hutuombea na kutusaidia kwa sababu anajua udhaifu wetu na hivyo hatupaswi kuogopa, kwa hiyo kuchochea kwetu hapa ni pamoja na kumtanguliza Mungu mbele katika kila tunalolifanya na Roho Mtakatifu atakuwepo kutusaidia kwa dhamiri njema!


Namna karama zinavyochochewa


Kwa kuwa Karama na vipawa hutoka kwa Mungu, ni lazima Mungu atangulizwe mbele, katika karama za maongozi ya kanisa na vipawa vya roho mtakatifu kamwe hatuwezi kutumia akili zetu wenyewe wala hatupaswi kutumia ngubvu zetu Roho Mtakatifu hufanya kazi na sisi kama tutakubalia atutumia kwa hiyo lazima kwetu kuwekewa Mikono na watumishi wa Mungu ili watuombee neema ya Mungu katikalile tunalokwenda kulifanya 

1.       2Timotheo 1;6 “Kwa sababu hiyo nakukumbusha, uichochee karama ya Mungu, iliyo ndani yako kwa kuwekewa mikono yangu.” 

     Viongozi wa kanisa wanapotuombea neema na kuweka mikono yao juu yetu kazi zile zilizowekwa mbele yetu zinapata kibali cha kiungu na karama zilizokuwa zimejificha huibuka, hekima na maarifa hutukalia na ndio maana mtu akiwekewa mikono na kubarikiwa mwenendo wa maisha yake huwa tofauti Matendo ya mitume 13: 1-3 “Na huko Antiokia katika kanisa lililokuwako palikuwa na manabii na waalimu, nao ni Barnaba, na Simeoni aitwaye Nigeri, na Lukio Mkirene, na Manaeni aliyekuwa ndugu wa kunyonya wa mfalme Herode, na Sauli. Basi hawa walipokuwa wakimfanyia Bwana ibada na kufunga, Roho Mtakatifu akasema, Nitengeeni Barnaba na Sauli kwa kazi ile niliyowaitia. Ndipo wakiisha kufunga na kuomba, wakaweka mikono yao juu yao, wakawaacha waende zao.” Mtu wa Mungu anapowekewa mikono na kuombewa neema kwaajili ya majukumu aliyopewa roho ya maarifa na hekima ya kutekeleza wajibu wake kwa uzuri hukaa juu yake Kumbukumbu la torati 34:9 “Na Yoshua, mwana wa Nuni, alikuwa amejaa roho ya hekima; maana Musa alikuwa amemwekea mikono yake juu yake; wana wa Israeli wakamsikiliza, wakafanya kama Bwana alivyomwamuru Musa.” Yoshua aliweza kuwa kiongozi shujaa na mwenye imani na akasikilizwa na wana wa Israel kwa kuwa aliwekewa mikono na Musa hivyo kwa kuwekewa mikono na kuombewa neema kamama zilizoko ndani yako zinaweza kuchochewa kwa msaada wa Roho Mtakatifu.


2.       Kubali kufundishwa 


1Timotheo 4:13 “Hata nitakapokuja, ufanye bidii katika kusoma na kuonya na kufundisha.Paulo Mtume pia alimwambia Timotheo afanye bidii sana katika kusoma, Tayari Timotheo alikuwa ni Muhubiri wa Injili na alikuwa ni mwangalizi wa makanisa lakini anatakiwa afanye bidii sana katika kusoma, uko ujuzi mwingi umejificha katika vitabu, lakini kutokana na watu wengi kuwa na uvivu wa kusoma na kuelimika wamezima moto au wameshindwa kuuchochea moto na kuchochea vipawa vyao, kila kitu duniani kinahitaji kujiongeza, wako watu wengi sana hawafurahii ndoa zao kwa sababu wanandoa wameridhika na hali ile ile na ujuzi uleule na hawataki kujaribu kujifunza na kutafuta mambo mengine kutoka vitabuni, wako wafanya biashara ambao biashara zao zimedumaa kwa sababu wana mbinu zilezile na mitindo ileile, wafanyakazi katika taasisi, walimu na kadhalika wanapaswa kujiongeza, serikali mara kadhaa katika sekta ya elimu wamebadili silabasi, mifumo ya mitihani, mbinu za ufundishaji bila kutoa semina  ya kutosha na kueleweka kwa kwa walimu, ili waendane na mfumo mpya na kuwapeleka katika ngazi ya juu, wapo wachungaji wamesoma zamani na mambo yamebadilika wanapaswa kupata semina elekezi katika Nyanja zao ili kujiongeza na kuchochea uelewa walio nao mpaka kuwapeleka ngazi nyingine kila ki[pawa karama na nafasi Mungu anayotupa inahitaji maarifa ya kutosha  na bidii katika kujifunza ili ifanyike kwa usahihi zaidi


Kuna baadhi ya karama na vipawa ambavyo Mungu ameweka ndani yetu ambavyo ili vifanye kazi na kunolewa na kutumika katika viwango vya juu lazima kusoma na kujisomea na kujiongeza kuhusike au mazoezi makali na miiko yake au nidhamu zake zihusike, siku hizi kumeibuka wimbi kubwa sala la watu wanaomtumikia Mungu huku wakiwa hawana mafunzo ya utumishi huo, huu ni msiba mkubwa sana nakubali kuwa utumishi ni huduma na ni karama na ni kipawa lakini kinaweza kufanya kazi vizuri kwa kupitia mafunzo aidha mafunzo rasmi au mafunzo yasiyo rasmi lakini ni muhimu kupitia mafunzo hayo kwa muda wa kutosha ili utumishi wetu uwe na ufanisi na hii ndio njia mojawapo ya kuichochea Karama, Mungu humtumia mtu vuziri zaidi baada ya kumuandaa kwa muda wa kutosha na mrefu zaidi Matendo ya Mitume 7:22Musa akafundishwa hekima yote ya Wamisri, akawa hodari wa maneno na matendo” Mungu alimtumia sana nabii Musa lakini Musa alikuwa msomi alifundishwa hekima yote ya wamisri na akawa Hodari wa maneno na matendo, ni kwa kusoma tunaweza kuchochea Karama zilizoko ndeani yetu na tukawa watu Hodari, lazima ufikie wakati tukubali kujifunza tuwasikilize walimu na kuwatii, tuwasikilize wazazi na kuwatii, tuwasikilize makocha na kuwatii, tujifunze kwa waliostaafu, tujifunze kwa waliotutangulia, tujifunze hata kwa walioshindwa kwa kuwauliza walishindwaje ili sisi tusipite katika njia ileile.  

Matendo 18:24-26 “Basi Myahudi mmoja, jina lake Apolo, mzalia wa Iskanderia, mtu wa elimu, akafika Efeso; naye alikuwa hodari katika maandiko. Mtu huyo alikuwa amefundishwa njia ya Bwana; na kwa kuwa roho yake ilikuwa ikimwaka, alianza kunena na kufundisha kwa usahihi habari za Yesu; naye alijua ubatizo wa Yohana tu. Akaanza kunena kwa ujasiri katika sinagogi; hata Prisila na Akila walipomsikia wakamchukua kwao, wakamweleza njia ya Bwana kwa usahihi zaidi.                 

Maandiko yanaonyesha jinsi Apollo alivyokuwa mtu mwenye Elimu na alikuwa hodari katika maandiko na alikuwa Muhubiri hata hivyo alihitaji kujua maswala kadhaa kwa usahihi zaidi na mwalimu wa neno la Mungu Prisilla na Akila ambao walikuwa ni watumishi wa Mungu Pamoja na Paulo mtume wao walimfundisha njia ya bwana kwa usahihi zaidi ili kuichochea huduma yake, Tunapokubali kujifunza tunajiweka katika kutumiwa na Mungu katika viwango bora zaidi na kusaidia kupunguza makosa ya kibinadamu, hivyo unapobaini kuwa una kipawa fulani tafuta watu sahihi watakaosaidia kukinoa ili kukiweka kitaalamu zaidi, ili utumiwe vema na kwa ubora zaidi.

3.       Hakikisha unaonana na watu sahihi.

Mungu anapokuwa ameweka Karama au kipawa au aina fulani ya maono, mwanzoni ni rahisi sana watu kukataa kutambua kipawa au karama uliyo nayo na unaweza kujikuta uko katika mazingira ya watu ambao wanaweza kuua kile ulicho nacho kwa nia njema au mbaya lakini pia kwa kutokujua kuwa umebeba nini, Nilipotembelea taifa la Korea ya kusini mwaka 2016 niliwahi kukutana na wat kadhaa wanaotumia mkono wa kushoto kwa ubora sana kama mimi na watanzania wenzangu tunaotumia mkono wa kulia, Mkorea mmoja akaniambia kuwa watu wanaotumia mkono wa kushoto ni wenye akili sana na hapa Korea wako wengi mno, kwa haraka nilisikia uchungu moyoni kabla ya kujibu lolote niliwaza kuwa ina maana sisi tunaotumia mkono wa kulia hatuna akili? Lakini haraka sana jibu llikuja na nikamwamboa mkorea yule kuwa kama ni hiyo Afrika watu wengi wana akili sana kwa sababu kila mtoto anayezaliwa na niliowaona mimi wanatumia mkono wa kushoto lakini wazazi wetu hutuchapa na kutukemea kisha hutufundisha kutumia mkono wa kulia kwa sababu kwetu Afrika kutumia mkono wa kushoto kwa mila na desturi zetu sio jambo la busara na halna heshima, na mkorea yule aliacha majivuno yake,  kwa nini nimetumia mfano huu hapa unaweza kuwa na kipawa cha aina fulani na unaweza kuwa umezaliwa nacho unaweza kuwa unapenda kuchora na wazazi wanaweza kudhani unajisomea kumbe unachora na wakakukataza kuchora ili kwamba usome lakini kumbe wanaua kitu cha thamani ulichojaliwa na Mungu, Unaweza kuwa unapenda sana kucheza mpira lakini wazazi wakakukataza ili kwamba usije ukaumia au uweze kuweka mkazo katika kusoma lakini kumbe wakawa wanafifisha kipawa kilichoko ndani yako!  Mtu mwenye karama au kipawa ili aweze kukichochea hana budi kuhakikisha kuwa anaelekea mahali sahihi ili kupata mafunzo na kutiwa moyo zaidi kuhusu kipawa chake ona katika  

Luka 1:39-40 “Basi, Mariamu akaondoka siku hizo, akaenda hata nchi ya milimani kwa haraka mpaka mji mmoja wa Yuda, akaingia nyumbani kwa Zakaria akamwamkia Elisabeti.”

 Unaweza kujiuliza kuwa ni kwa nini Mariamu alipotaarifiwa  na Malaika Gabriel kuwa atakuwa na Mimba na atamzaa Masihi ambaye ni mrithi wa kiti cha enzi cha Daudi milele? Na tunaona Mariamu anafanya haraka kwenda kumtembelea Elizabeth na kukaa kwake miezxi mitatu wakati malaika anamwambia jambo hili Mariamu pia alimueleza jambo jingine kwa kusudi la kumtia moyo Mariamu maana alijiuliza inawezekanaje jambo hili kutokea naye hajui mume? Malaika alitaka kumuonyesha Mariamu kuwa Mungu hashindwi jambo na hata Elizabeth aliyeitwa tasa sasa ana ujauzito wa miezi sita ona:-

Luka 1:34-37 “Mariamu akamwambia malaika, Litakuwaje neno hili, maana sijui mume? Malaika akajibu akamwambia, Roho Mtakatifu atakujilia juu yako, na nguvu zake Aliye juu zitakufunika kama kivuli; kwa sababu hiyo hicho kitakachozaliwa kitaitwa kitakatifu, Mwana wa Mungu. Tena, tazama, jamaa yako Elisabeti naye amechukua mimba ya mtoto mwanamume katika uzee wake; na mwezi huu ni wa sita kwake yeye aliyeitwa tasa; kwa kuwa hakuna neno lisilowezekana kwa Mungu.” 


Unaona Jambo hili lilimfanya Mariamu kwenda haraka sana kwa Elizabeth kwa sababu alikuwa amechanganyikiwa kwa maono makubwa ambayo malaika alisema naye ni kama malaika alikuwa amemuonyesha wazi kuwa mtu sahihi anayeweza kukusaidia kwa wakati huu ni Elizabeth ambaye naye Mungu amemfanyia mambo makubwa na magumu yaliyoshindikana kibinadamu Mariamu hangeweza kumwambia mama yake. Wala mwalimu wake au mtu yeyote aliyemjua alijua kuwa mtu aqnayeweza kumuelewa ni Elizabeth tu mtu mwenye maono na ndoto na muujiza na kipawa na karama kama zake 


Luka 1:36-37” Tena, tazama, jamaa yako Elisabeti naye amechukua mimba ya mtoto mwanamume katika uzee wake; na mwezi huu ni wa sita kwake yeye aliyeitwa tasa; kwa kuwa hakuna neno lisilowezekana kwa Mungu.Mariamu alikuwa ametiwa moyo kupitia maneno haya alihitaji kujifunza kwa mtu sahihi aliyemtangulia alihitaji muongozo, alihitaji kupokea uzoefu, Elizabeth ndiye aliyekuwa mtu sahihi wakati huu wa kumtia moyo Mariamu, kumfundisha, kumuelekeza, kumuonyesha upendo na urafiki, kumpandisha imani na kumtetea ona maneno ya Elizabeth 

Luka 1:41-45 “Ikawa Elisabeti aliposikia kule kuamkia kwake Mariamu, kitoto kichanga kikaruka ndani ya tumbo lake; Elisabeti akajazwa Roho Mtakatifu; akapaza sauti kwa nguvu akasema, Umebarikiwa wewe katika wanawake, naye mzao wa tumbo lako amebarikiwa. Limenitokeaje neno hili, hata mama wa Bwana wangu anijilie mimi?  Maana sauti ya kuamkia kwako ilipoingia masikioni mwangu, kitoto kichanga kikaruka kwa shangwe ndani ya tumbo langu. Naye heri aliyesadiki; kwa maana yatatimizwa aliyoambiwa na Bwana.”   


Unadhani Mariamu angeenda kwa mtu asiye sahihi ingekuwaje angeambiwa Mungu wangu ni nani atakayekuelewa umekwisha unaanzaje kumwambia mtu una mimba unawezaje kutimiza ndoto hii unawezaje kuifanya biashara hii, unawezaje kuandkia andiko maoni haya ndugu yangu hii ni kazi ngumu sana haiwezekani, vifaa vimepanda sana haiwezekani, ujenzi ni gharama mno hutaweza unapokuwa na karama au ndoto au maono enenda  kwa mtu sahihi Elizabeth anamwambia Mariamu tena akiwa amejaa Roho Mtakatifu Naye heri aliyesadiki; kwa maana yatatimizwa aliyoambiwa na Bwana.”   Elizabeth anamwambia mariamu ulichoambiwa na Mungu kitatimia tu na ni baraka kubwa kama utaamini, mwamini Mungu yeye anaweza ndipo Mariamu akamuadhimisha Mungu na kutulia kwa Elizabeth kwa miezi mitatu, Unapokuwa na njozi au hata mapito na majaribu enenda kwa watu wanaopitia majaribu kama yako mtazungumza lugha moja, unapokuwa na karama waone waliokutangulia  walio sahihi wenye kipawa kama chako jifunze kutoka kwao ambao lugha zao zitakuwa chanya watakuambia UTATOBOA TU, Mwanangu utatoka hii kitu nakuhakikishia utatoka kirahisi tu, hivyo ndivyo unavyoweza kuichochea karama iliyo ndani yako.


4.       Kuwa mkomavu.

Acha ulimbukeni, watu wengi sana wameua vipawa vyao kwa sababu ya ulimbukeni, vipawa vinapowapa mafanikio wanakuwa na mbwembwe nyingi, kiburi kinapanda na kujidai, wakijifikiri kuwa wao ni watu maarufu sana wanapoteza adabu na kujali utu, wanaongeza mbwembwe nyingi sana, wanakosa umakini,  na wanaacha kujilinda Kipawa ni zawadi ni uwakili ni amana ambayo Mungu amewekeza ndani yako lazima uilinde 2Timotheo 1:14 “Ilinde ile amana nzuri kwa Roho Mtakatifu akaaye ndani yetu.”  Unawezaje kujilinda kuhakikisha kuwa uko vilevile au unazidi mno lazima ujilinde na kiburi, watu wenye mafanikio sana duniani wala hawajidai,  Hawana maringo, hawajifanyi wanajua, wanapokea ushauri, wanajali wengine. Ni vema tukajivika unyenyekevu kwa sababu njia ya Mungu ya kutupeleka juu ni kujishusha 1Petro 5:6 

Basi nyenyekeeni chini ya mkono wa Mungu ulio hodari, ili awakweze kwa wakati wake;”  Kumbe kanuni ya Mungu ya kukukweza ni kujishusha na kuishi maisha ya unyenyekevu. Unyenyekevu ndio unaoonyesha ukomavu lakini tukiwa na kiburi ni muhimu kufahamu kuwa hatuko mbali na aibu Mitahli 11:2 “Kijapo kiburi ndipo ijapo aibu; Bali hekima hukaa na wanyenyekevu. Watu wengi wenye vipawa na karama   wameharibu sifa zao kwa sababu ya kiburi na hivyo wamefupisha muda wao wa kumtumikia Mungu au kutimiza kusudi walilokusudiwa na Mungu duniani ni kutokana na kujinyenyekeza sana Yesu aliinuliwa sana hii ndio kanuni ya mafanikio ya kutunza kipawa chako mbele za Mungu na wanadamu nia nyenyekevu itakuweka juu kama ilivyomuweka yesu juu mno Wafilipi 2:5-11” Iweni na nia iyo hiyo ndani yenu ambayo ilikuwamo pia ndani ya Kristo Yesu; ambaye yeye mwanzo alikuwa yuna namna ya Mungu, naye hakuona kule kuwa sawa na Mungu kuwa ni kitu cha kushikamana nacho; bali alijifanya kuwa hana utukufu, akatwaa namna ya mtumwa, akawa ana mfano wa wanadamu; tena, alipoonekana ana umbo kama mwanadamu, alijinyenyekeza akawa mtii hata mauti, naam, mauti ya msalaba. Kwa hiyo tena Mungu alimwadhimisha mno, akamkirimia Jina lile lipitalo kila jina; ili kwa jina la Yesu kila goti lipigwe, la vitu vya mbinguni, na vya duniani, na vya chini ya nchi; na kila ulimi ukiri ya kuwa YESU KRISTO NI BWANA, kwa utukufu wa Mungu Baba.” 


5.       Usikubali kupoa
 

Tunaweza kuchochea karama vilevile kwa kuhakikisha kuwa hatuuzimi moto wa Mungu ulioko ndani yetu, usikubali kupoa au kuwa vuguvugu, Maandiko yanaonyesha kuwa Mungu akikupa amekupa na haondoi kipawa wala karama alizoweka ndani yetu lakini ni kwa nini watu hufulia na kuisha kabisa sababu kubwa ni kupoa au kuwa vuguvugu Mungu anachukizwa sana na watu vuguvugu maandiko yanaonyesha uwezo wa kupoa uko katika mikono yetu na uwezo wa kuwa Moto pia, Mungu ameweka karama ndani yako wewe ni wajibu wako kuhakikisha unabaki moto Ufunuo 3:15-16 “Nayajua matendo yako, ya kuwa hu baridi wala hu moto; ingekuwa heri kama ungekuwa baridi au moto. Basi, kwa sababu una uvuguvugu, wala hu baridi wala moto, nitakutapika utoke katika kinywa changu.” Unaona Mungu hapendezwi na watu vuguvugu hii maana yake anatujua vema anataka tuwe moto, au ukishindwa uwe baridi ijulikana umekwisha umepoa lakini kamwe Mungu hataki tuwe vuguvugu atakutapika ndio maana utaweza kuona watu wanaibuka kisha wanatokweka na karama na vipawa vinakwisha. 


6.       Usimzimishe Roho Mtakatifu.

Biblia inaeleza katika 1Wathesalonike 5:19 “Msimzimishe Roho;” Roho Mtakatifu ni Mungu na ndiye chanzo cha Karama na vipawa vyote anavyowapa wanadamu, Kumzimisha Roho Mtakatifu maana yake nini  Roho Mtakatifu kama Mungu Hakuna mtu anaweza kumzimisha  haiwezekani lakini sisi wenyewe tena tunaweza kuanza kumuhuzunisha Roho wa Mungu kutokana na mtindo wa maisha unaomuhuzunisha Roho Mtakatifu kama Mungu na kumfanya aondoe neema yake Waefeso 4:30 “Wala msimhuzunishe yule Roho Mtakatifu wa Mungu; ambaye kwa yeye mlitiwa muhuri hata siku ya ukombozi.”  Tunapofanya dhambi na uasi endelevu dhidi ya Mungu Roho wa Mungu anaweza kutuacha na ushujaa wetu utakuwa umefikia kikomo na ndio maana Daudi aliomba asiondolewe Roho Mtakatifu Zaburi 51:11 “Usinitenge na uso wako, Wala roho yako mtakatifu usiniondolee.” Kwa Msingi huo tukiishi mtindo wa maisha unaomnyima Mungu Roho Mtakatifu kutuongoza na kutusaidia huku yeye akiwa chanzo cha vipawa vyetu tutapoteza uwepo wake Napenda sana tafasiri ya Kiibrania ya neno Msimzimishe Roho wenyewe wanatumia neno “KABAH” sawa na kusema Msimkabe Roho Mtakatifu, Msimbanie, kiingereza Do note Expelled, au do not neglected  au Quench not,  Kwa maana hiyo sisi wenyewe ndio tunawajibu wa kujiachia katika neema ya Mungu, kwa kufunga, kuomba, kusoma neno, kuabudu, kujiweka karibu na Mungu kuutafuta uso wake kwa bidii, kutubu kwa haraka endapo tumekosea na tutaona Roho wa Mungu alkiendelea kukifungua kipawa kilichopo ndani yetu kidogo kidogo. Na kututumia kwa viwango vikunbwa na vya hali ya juu.

7.       Uwe hodari

Watu wenye vipawa wanapigwa vita sana wanapambana watu wenye wivu, Ibilisi pia hapendi kwa sababu karama ni silaha za maangamizi zinampa Mungu utukufu na kuharakisha kazi ya Mungu na kwa sababu hizo upinzani ni lazima, Karama na vipawa pia Mungu huzitumia kuinua maisha binaksi ya Muhusika kwaajili ya hayo ni lazima uwe hodari na uwe shujaa Yoshua 1:9 “Je! Si mimi niliyekuamuru? Uwe hodari na moyo wa ushujaa; usiogope wala usifadhaike; kwa kuwa Bwana, Mungu wako, yu pamoja nawe kila uendako.” Mungu anataka tuwe hodari na tuwe na moyo wa ushujaa kwa sababu anajua kuna changamoto mbele yetu, Kila mtu anayetaka kuzichochea karama akumbuke kuwa mbali na hofu na awe na ujasiri, kwa sababu kila utakapoitumia Karama uliyonayo kutainuka wasiopendezwa na watajaribu kwa kila jinsi na kila namna kupingana nawe kama nduguze Yusufu walivyochukizwa naye hata kutaka kumuua kwaajili ya ndoto  alizokuwa nazo  

Mwanzo 37:5-11 “Yusufu akaota ndoto, akawapa ndugu zake habari, nao wakazidi kumchukia;  akawaambia, Tafadhalini, sikieni ndoto hii niliyoiota. Tazama, sisi tulikuwa tukifunga miganda shambani, kumbe! Mganda wangu ukaondoka ukasimama, na tazama, miganda yenu ikazunguka ikainama mbele ya mganda wangu. Ndugu zake wakamwambia, Je! Kweli wewe utatumiliki sisi? Nawe utatutawala sisi? Wakazidi kumchukia kwa ajili ya ndoto yake, na kwa maneno yake. Akaota tena ndoto nyingine, akawaambia ndugu zake, akasema, Angalieni, nimeota ndoto nyingine; na tazama, jua na mwezi na nyota kumi na moja zikaniinamia. Akawaambia baba yake na ndugu zake; baba yake akamkemea akamwambia, Ni ndoto gani hii uliyoiota? Je! Mimi na mama yako na ndugu zako tutakuja tukusujudie hata nchi?  Ndugu zake wakamhusudu; bali baba yake akalihifadhi neno hili.Unaweza kuona Mungu anampa ndoto Yusufu kuwa mtawala, ana maono mazito kwaajili ya kuja kuisaidia familia yake ana karama ya maongozi, ana karana ya unabii na kipawa cha kutafasiri ndoto kipawa hiki kingembeba na kumpeleka kwenye kiwango kingine kingeisaidia jamii na ndugu nzake pia lakini wao ndio walikuwa wa kwanza kuona wivu na hata kutaka kumuua kabisa ona 

Mwanzo 37:18-20 “Wakamwona toka mbali, na kabla hajawakaribia, wakafanya shauri juu yake ili wamwue. Wakasemezana wao kwa wao, Tazama, yule bwana wa ndoto anakuja. Haya, twende, tukamwue na kumtupa katika birika mojawapo, nasi tutasema, Mnyama mkali amemla; kisha tutaona zitakuwaje ndoto zake.” 


 Unaweza kuona ndugu zake Yusufu walikusudia kumuua kwa sababun ya ndoto zake yaani ileile karama aliyopewa iliwavutia maadui, ningeweza kukupa mifano Mingi kama Daudi alivyotaka kuuawa na Sauli kwa sababu ya karama, ningeweza kukupa mfano wa Samsoni alivyowindwa na Wafilisti kutokana na ngvu zake na uwezo wake wa ajabu aliokuwa nao, ningekueleza jinsi Yesu alivyokuwa tishio kwa viongozi wa dini sio kwa sababu alikuwa mwovu bali kwa wema uliovutia watu kwa maelfu yao na miujiza mikubwa aliyoifanya, ningekuopa habari za Petro na Yohana walivyokutana na uopinzani kwa sababu ya muujiza mashuhuri walioufanya, sikwambii habari za Paulo aliyetumiwa kufanya miujiza na kuwavuta wengi kwa Yesu alivyotaka kuuawa,  sikwambii habari za Daniel ambaye alifanyiwa njama za kila namna kutokana na vipawa alivyokuwa navyo, sikwambii Michael Jakcson alivyochukiwa na wazungu na kufanyiwa kila aina ya hila kutokana na vipawa,  haya na mengineyo ni mifano ni mifano tu inayokutaka uwe makinina uhakikishe unakuwa na ushujaa na moyo mkuu ili kutokuizima ile karama iliyoko ndani yako! Kipawa na karana zina tabia ya kuvutia watu wema na wabaya  


Luka 11: 53-54 “Alipotoka humo, waandishi na Mafarisayo walianza kumsonga vibaya, na kumchokoza kwa maswali mengi, wakimvizia, ili wapate neno litokalo kinywani mwake.” Unaweza kuona namna na jinsi waandishi yaani walimu nwa sheria na Mafarisayo walivyokuwa wakimzongazonga Yesu na kumchokoza ili waweze kumsonga kwa maswali mengi kusudi lao kuu ni kupata neno la Kumshitaki, ili kumuharibia Mungu akupe hekima na Busara  kama alivyompa Yesu ili kujilinda na kujihami na maadui.

Kwa sababu hiyo nakukumbusha, uichochee karama ya Mungu, iliyo ndani yako kwa kuwekewa mikono yangu

Na Rev. Innocent Kamote.

Mkuu wa wajenzi mwenye hekima!

0718990796