Jumapili, 7 Agosti 2016

Toka mautini mpaka Mezani kwa Bwana!


Yohana 11:32-44: 12:1-2
 
32.Basi Mariamu alipofika pale alipokuwapo Yesu, na kumwona, alianguka miguuni pake, akamwambia, Bwana, kama ungalikuwapo hapa, ndugu yangu hangalikufa. 33. Basi Yesu alipomwona analia, na wale Wayahudi waliofuatana naye wanalia, aliugua rohoni, akafadhaika roho yake, 34. akasema, Mmemweka wapi? Wakamwambia, Bwana, njoo utazame. 35. Yesu akalia machozi. 36. Basi Wayahudi wakasema, Angalieni jinsi alivyompenda. 37. Bali wengine wao wakasema, Je! Huyu aliyemfumbua macho yule kipofu, hakuweza kumfanya na huyu asife? 38. Basi Yesu, hali akiugua tena nafsini mwake, akafika kwenye kaburi. Nalo lilikuwa ni pango, na jiwe limewekwa juu yake. 39. Yesu akasema, Liondoeni jiwe. Martha, dada yake yule aliyefariki, akamwambia, Bwana, ananuka sasa; maana amekuwa maiti siku nne. 40. Yesu akamwambia, Mimi sikukuambia ya kwamba ukiamini utauona utukufu wa Mungu? 41. Basi wakaliondoa lile jiwe. Yesu akainua macho yake juu, akasema, Baba, nakushukuru kwa kuwa umenisikia. 42. Nami nalijua ya kuwa wewe wanisikia sikuzote; lakini kwa ajili ya mkutano huu wanaohudhuria nalisema haya, ili wapate kusadiki kwamba ndiwe uliyenituma. 43. Naye akiisha kusema hayo, akalia kwa sauti kuu, Lazaro, njoo huku nje.  44. Akatoka nje yule aliyekufa, amefungwa sanda miguuni na mikononi, na uso wake amefungwa leso. Naye Yesu akawaambia, Mfungueni, mkamwache aende zake.”

“1. Basi, siku sita kabla ya Pasaka, Yesu alifika Bethania, alipokuwapo Lazaro, yeye ambaye Yesu alimfufua katika wafu. 2. Basi wakamwandalia karamu huko; naye Martha akatumikia; na Lazaro alikuwa mmojawapo wa wale walioketi chakulani pamoja naye.”

 Kaburi la Mtakatifu Lazaro huko Bethania Nchini Israel

Utangulizi:

Vifungu hivi vya Biblia ni moja ya vifungu vya kushangaza sana katika Biblia,Ni kifungu kinachotupa wasomaji wa Biblia nafasi ya kuona Nguvu, utukufu na fahari ya Yesu Kristo na Uweza wake, Hapa tunamuona mtu anayeitwa Lazaro akifufuliwa toka mautini mpaka kukaa karamuni mezani na Bwana.
Katika kifungu hiki tunaona kile ambacho Yesu alikifanya kwa Lazaro, na hiki ndicho anachowqeza kukifanya pia kwa wale waliopotea au kufia dhambini, Kifungu kinatuonyesha jinsi Yesu alivyo na uwezo wa kukutoa katika hali mbaya na kukualika katika Karamu pamoja naye katika hali yoyote ile uliyonayo yenye kuashiria kufa na kuharibika kwa kila kitu katika hali ya mauti Yesu anao uwezo wa kukuleta katika furaha na uchangamfu.

Mstari 32-42 Hali ya Lazaro.

Alikuwa masikini na mtu aliyechakaa, aliugua kwa muda mrefu na sasa amekufa hayuko hai tena, alikuwa sasa kaburini, Familia ndugu na jamaa walikuwa wamekusanyika kwa msiba na maombolezo, Yeye hangeliweza kuwasikia kwa vile amefariki, Hata Yesu alipolisogelea Kaburi lake asingeliweza kusikia kitu wala kuhisi uwepo wa Bwana, hii inaweza kuwa hali ya kila mtu ambaye hajamwamini Yesu ni mfu mbele za Mungu Waefeso 2:1 Nanyi mlikuwa wafu kwa sababu ya makosa yenu ndivyo Biblia isemavyo, Dhambi hutufanya tusihisi uwepo wa Mungu, hatuwezi kumjibu mungu lolote katika hali ya uovu na dhambi, wala hatuwezi kuwa na ushirika naye wala na wenzetu, Lazaro alikuwa amekufa na amezikwa.

Alikuwa ameoza kwa mujibu wa Maelezo ya Martha Lazaro alikuwa amekufa siku nne sasa alikuwa ameanza kuharibika, kama ni hatua ya kifo imekwenda mbali zaidi, Yesu alikuwa amefufua watu kadhaa ambao walikuwa wamekufa Luka 8 alimfufua binti wa Yairo na Luka 7 alimfufua kijana wa mjane huko naini, wote hao walikuwa wamekufa lakini walikuwa hawaanza kuoza labda walikuwa wamekufa saa chache tu, lakini sivyo ilivyo kwa Lazaro alikuwa amekufa na alikuwa amezikwa na sasa ameoza, Wakati Yesu anafika Kaburini alikozikwa lazazo ilikuwa zimepita siku nne sasa alikuwa ananuka, alikuwa amekufa kiasi ambacho kila mtu alikubali kuwa amekufa,kifo cha kimwili nafuu yake ni mazishi tu na kifi cha kiroho nafuu yake ni Jehanamu tu Warumi 6:23.

Lazaro alikuwa ni maiti iliyoharibika.

Unapomsikiliza Martha na Mariam Mstari wa 21,32,36 unaweza kupata wazo lililowazi kabisa kuwa Lazaro alikuwa ni maiti iliyofikia hatua ambayo hakuna lingine linaloweza kufanyika na wote tunaweza kukubaliana kuwa huo ndio uhalisia, kisayansi na kitaalamu, Lakini kitu cha kushangaza ni huyu mwanaume anayeitwa Yesu, huyu yeye anauwezo wa kufanya mambo kuwa tofauti, watu wanaweza kukuweka kaburini na hata kukukatia tamaa na inawezekana kabisa hata ndugu zako wakakubaliana kabisa kuwa wewe mambo yako hayawezekani tena, tabia zako, hali yako, mwenendo wako, Biashara zako, Masomo yako, magonjwa yako, ndoa yako, kila mtu akasema haiwezekani tena, huinuki tena, hutoki tena,basi tena wakakuweka kaburini, na kutokutaka kukusogelea huko wakaombolezea kwa mbali, lakini yuk mmoja ambaye anaweze kubadilisha mazingira anaweza kumuinua myonge kutoka jalalani, anaweza kufufua nafsi yako anaweza kurejesha matumaini yaliyokufa, anaweza kufanya tofauti katika maisha yako, anaweza kufanya yasiyowezekana yakawezekana, anaweza kugeuza huzuni yako kuwa furaha, msiba wako kuwa Harusi,kunuka kwako kuwa kunukia, kukataliwa kwako kuwa kukimbiliwa, kuchokwa kwako, kuwa kibali, kukimbiwa kwako kuwa kukimbiliwa Ni Yesu ni Yesu ni Yesu pekee anayeweza kufanya tofauti katika maisha yako, kuna uwezekano ukawa umekata tamaa na watu wakakukatia tamaa lakini habari njema leo ni kuwa Yesu analikaribia kaburi lako, Yeye ndiye pekee anayeweza kufanya tofauti katika matumaini yaliyokufa Matendo 4:12, Yohana 14:6, Yesu alilisogelea kaburi la mtu aliyeachwa peke yake, ananuka, ameoza, ameshindikana yuko gizani na kubadilisha mfumo wa Mambo.

43-44 Yesu alimuita Lazaro.

Yesu alipokwenda Kaburini alimuita Lazaro tu, najua kulikuwa na sababu maalumu angesema ewe uliyekufa amka njoo huku wafu wote wangefufuka, Yesu alikuwa na akili sana alimuita yule aliyemkusudia tu, wakati wote Mungu anapoita pia kupitia ujumbe maalumu kama huu, anamuita mtu mmoja binafsi huyu ataguswa na mwito huu, wapezni wito wa Mungu sio wa jumlajumla Mungu anamakusudi na kila mmoja wetu kwa jinsi yake ni imani yangu kuwa Yesu anamakusudi na ujumbe huu kwa mtu Fulani na ni lazima aguswe, Mungu anataka watu wote waokolewe 1Timotheo 2:4, na kila atakayeliitia jina la Bwana ataokolewa Warumi 10:13, Ufunuo 22:17, mLakini yesu alikuja kuokokoa kile kilichopotea Luka 10:19 yuko mtu ujumbe huu unamuhusu.

Yesu alimuita Lazazo na ni Lazaro aliyetoka kaburini alipoitwa, Mungu anakuita katika wokovu, katika uponyaji, katika wito wa kumtumikia Mungu, anakuita kutoka katika shida zako na mahitaji yako anakuita wewe amekuona wewe anataka kukusaidia wewe Toka huku nje, ondoka kaburini, ondoka gizani yuko Mwanaume anayekuita leo huyu ni Yesu

Lazaro alipoitwa nini kilitokea?

·         Uhai ulirudi ndani yake
·         Aliwekwa huru baada ya kufunguliwa sanda zake
·         Aliona nuru kuu kwani kaburini ilikuwa giza
·         Aliishi maisha ya raha na alikuwa na wakati wa kufurahia maisha sasa alialikwa karamuni na kula na Bwana Yesu 

 Yesu yuko tayari kumuita kila mmoja wetu toka Kaburini mwake, swali la kujiuliza je tuko tayari kuhudumiwa naye, je tuko tayari kuisikiliza Sauti yake?yuko tayari kukupa wokovu, kukuhudumia na kukutumia yeye bado anaita, kama uhusiano wako nay eye umeharibika anakuita mtengeneze ili akualike karamuni mwake naye atakutoa mautini mpaka mezani pake.

Mkuu wa Wajenzi mwenye Hekima!
Rev. Innocent Kamote
0718990796

Hakuna maoni: