Jumatatu, 10 Oktoba 2022

Vazi la Yusufu!


Mwanzo 37:23-24Ikawa Yusufu alipofika kwa ndugu zake, wakamvua Yusufu kanzu yake, kanzu ile ndefu aliyoivaa, wakamtwaa wakamtupa katika birika; na hiyo birika ilikuwa tupu, hamna maji.


Utangulizi:

Mojawapo ya viongozi wa kiroho ambao habari zao zimeandikwa kwa urefu sana katika maandiko ni pamoja na Yusufu, Yusufu anahesabika kama moya ya mababa wa Israel, ukiacha Abrahamu, Isaka na Yakobo, yeye ndio sababu kubwa kwa wana wa Israel kushuka Misri, kuna mambio mengi sana ya kujifunza katiika maisha ya Yusufu lakini moja wapo ya jambo la msingi na la muhimu sana tunalotaka kulizungumzia leo tena kwa kina ni pamoja na Vazi la Yusufu, vazi lake na nguo zake zinaonekana kuwa na mvuto wa kipekee na vilevile kuwa sababu ya mapito yake kuna nini kilipelekea hawa watu kumtenda machungu kisa kikianzia kwenye vazi? Maandiko yanasema hivi;-

Mwanzo 49:22-24 “Yusufu ni mti mchanga wenye kuzaa, Mti mchanga wenye kuzaa karibu na chemchemi, Matawi yake yametanda ukutani. Wapiga mishale walimtenda machungu, Wakamtupia, wakamwudhi, Lakini upinde wake ukakaa imara, Mikono yake ikapata nguvu, Kwa mikono ya Mwenye Enzi wa Yakobo; Kwa jina la mchungaji, yeye jiwe la Israeli,”

Maandiko hayatuambii kuwa Yusufu aliwakosea Ndugu zake, lakini yaonekana wazi kuwa ndugu zake walichukizwa naye na sababu kubwa inaweza kuwa ni wivu wenye uchungu na hasira kali juu yake, lakini Bwana alikuwa pamoja naye, matukio ya aina hii yanaweza pia kuwako katika jamii inayotuzunguka leo, tunaweza kujikuta katika wakati mgumu sana kwa sababu ya mafanikio ya aina mbalimbali na wakati mwingine kwa sababu ya kusudi la Mungu lililoko ndani yetu!  Na anayepingana na kusudi hilo kwa vyovyote vile ni adui Shetani ambaye wakati mwingine anaweza kuwatumia watu tena watu wa karibu.

Vazi la Yusufu!

Kisa cha kusikitisha cha maisha machungu ya Yusufu kinaanzia na namna Yusufu alivyonunuliwa na kuvishwa vazi la thamani kubwa sana na baba yake biblia inaelezea vazi hilo katika

Mwanzo 37:3-4 “Basi Israeli akampenda Yusufu kuliko wanawe wote, maana ni mwana wa uzee wake, akamfanyia kanzu ndefu. Ndugu zake wakaona ya kuwa baba yao anampenda kuliko ndugu zake wote, wakamchukia, wala hawakuweza kusema naye kwa amani.”

Maandiko yanaelezea kuhusu kanzu hii ndefu, na matoleo mengine ya kibiblia yanaitaja kama nguo yenye rangi nyingi, vazi hili la thamani lilikuwa ni vazi la gharama kubwa na kwa mujibu wa historia ya kibiblia lilikuwa ni vazi lililoweza kumtambulisha mtu kuwa ni mwana mfalme au mwana wa kifalme (Prince au Princess)

2Samuel 13:18 “Naye alikuwa amevaa kanzu ndefu; kwa kuwa kwa nguo hizo huvikwa binti za mfalme waliokuwa wanawali. Ndipo mtumishi wake akamleta nje, akafunga mlango nyuma yake.”

Kanzu hii au vazi kinabii ilikuwa inaashiria kuwa Israel au Yakobo amekusudia kumpa heshima kubwa na ya tofauti mwanaye aliyeitwa Yusufu, na kuanza kumfunza Yusufu kuwa mtawala na mfalme, Vazi hili alilotengenezewa na baba yake lilikuwa ni ishara ya upendeleo, neema na heshima maalumu aliyokuwa ametunukiwa Yusufu aidha na baba yake au na Mungu lakini kwa vile baba yake alikuwa nabii alikuwa anaashiria kuwa Yusufu hakuwa mtu wa kazi ngumu yeye alikuwa ni msimamizi na mwangalizi na kazi zake ni usimamizi kwani vazi lile halikuwa vazi la kazi bali vazi la kitawala! Lilikuwa ni vazi la kibali, kupendwa na neema ya Mungu

Vazi maalumu kwa Yusufu!          

Kwa nini Yakobo alimtengenezea Yusufu vazi maalumu? Maandiko yanaonyesha kwanza kabisa Kuwa Yakobo alimpenda Raheli sana kuliko Lea, jambo hili linaweza kuwa lilionekana wazi kwa watoto wa Yakobo ambao waliona wazi kuwa mama zao hawakupendwa kama alivyopendwa mama yake Yusufu,

Mwanzo 29:30-31 “Akaingia kwa Raheli naye, akampenda Raheli kuliko Lea, akatumika kwa ajili yake miaka saba mingine. BWANA akaona ya kwamba Lea hakupendwa, naye akafungua tumbo lake; bali Raheli alikuwa hazai.”

Unaona kwa hiyo ni wazi kuwa kutokana na Yakobo kumpenda sana Raheli kuliko Lea ilikuja kuwa rahisi vilevile kwa Yakobo kumpenda Yusufu kuliko watoto wengine japo hii ni dhana tu ya kibiblia na kitheolojia  

Mwanzo 30:22-24 “Mungu akamkumbuka Raheli; Mungu akamsikia, akamfungua tumbo. Akapata mimba, akazaa mwana, akasema, Mungu ameondoa aibu yangu. Akamwita jina lake Yusufu, akisema, BWANA aniongeze mwana mwingine.”

Raheli alipokuja kumzaa Yusufu pia alimpa jina Yufufu ambalo maana yake Bwana ameniondolea aibu yangu, kwa msingi huo kinabii pia mtoto huyu alikuwa anahusika na kuondoa aibu ya mama yake wote tutakuwa tunakumbuka kuwa mara baada ya anguko la Mwanadamu katika bustani ya Edeni Adamu na Eva walijisikia aibu, walijiona wako uchi na Mungu aliwatengenezea vazi ili kuifunika aibu yao au kuwaondolea aibu kumbuka

Mwanzo 3:21 “BWANA Mungu akawafanyia Adamu na mkewe mavazi ya ngozi, akawavika.” Yakobo alichokifanya kwa Mwanaye Yusufu, na jina alilopewa Yusufu na Vazi alilotengenezewa baadaye na Yakobo yalikuwa na maana sawa na kile Mungu alimfanyia Adamu na mkewe kwa kuwavika mavazi ya kuwaondolea aibu, maana yake Mungu aliwapa Heshima iliyokuwa imepotea na vilevile Yusufu kutengenezewa vazi lile maalumu ilikuwa ni Ishara ya Heshima kubwa kwake!,  na kinabii ni kijana ambaye angekuja kuiondolea aibu familia yake na kuiifadhi wakati wa dhiki, ukiacha heshima hii kijana huyu alikuwa mwadilifu na alijifunza mambo mengi kuhusu Mungu kutoka kwa baba yake na mara kwa mara ndiye aliyekuwa akitoa ripoti ya taarifa ya watoto wote wa Yakobo kwa  na kwa bahati mbaya wengi wao hawakuwa na tabia njema mwanzoni  ukilinganisha na Yusufu ona,

Mwanzo 37:2 “Hivi ndivyo vizazi vya Yakobo. Yusufu, aliyekuwa mwenye miaka kumi na saba, alikuwa akichunga kondoo pamoja na ndugu zake; naye alikuwa kijana pamoja na wana wa Bilha, na wana wa Zilpa, wake wa baba yake. Yusufu akamletea baba yao habari zao mbaya.”

Kwa hiyo utaweza kuona kutokana na usafi wa Yusufu, alionekana kama kikwazo kikubwa cha matendo maovu ya kaka zake, pia alionekana kama mbeya kwa sababu angeleleza taarifa zao mbaya walizokuwa wakizifanya, achilia mbali Ndoto zake za kiutawala ambazo zilikuja kuongeza chuki kubwa kwani sio tu, baba yake alikusudia kumuheshimu sana Yusufu, lakini sasa inaonekana kuwa hata Mungu alikuwa amekusudia kumuheshimu sana Yusufu kuliko nduguze na kumuinua juu kiutawala ona.

Mwanzo 37:5-11 “Yusufu akaota ndoto, akawapa ndugu zake habari, nao wakazidi kumchukia; akawaambia, Tafadhalini, sikieni ndoto hii niliyoiota. Tazama, sisi tulikuwa tukifunga miganda shambani, kumbe! Mganda wangu ukaondoka ukasimama, na tazama, miganda yenu ikazunguka ikainama mbele ya mganda wangu. Ndugu zake wakamwambia, Je! Kweli wewe utatumiliki sisi? Nawe utatutawala sisi? Wakazidi kumchukia kwa ajili ya ndoto yake, na kwa maneno yake. Akaota tena ndoto nyingine, akawaambia ndugu zake, akasema, Angalieni, nimeota ndoto nyingine; na tazama, jua na mwezi na nyota kumi na moja zikaniinamia. Akawaambia baba yake na ndugu zake; baba yake akamkemea akamwambia, Ni ndoto gani hii uliyoiota? Je! Mimi na mama yako na ndugu zako tutakuja tukusujudie hata nchi? Ndugu zake wakamhusudu; bali baba yake akalihifadhi neno hili.”

Ndoto za Yusufu ulikuwa ni unabii maalumu kutoka kwa Mungu kuwa Mungu angemuheshimu sana Yusufu na kuwa kwa vyovyote vila angekuja kuwatawala nduguze, sawa tu na baba yake alivyomtengenezea vazi maalumu, ni wazi kuwa Mungu alikuwa amekusudia kumuheshimu Yusufu, kila mmoja wetu kuna jambo ambalo kwalo Mungu amekusudia kukufanya maalumu kuliko wengine kuna heshima ambayo Mungu ameikusudia kwako wakati wote Mungu ana mpango mwema kwaajili yako

Yeremia 29:11 “Maana nayajua mawazo ninayowawazia ninyi, asema Bwana, ni mawazo ya amani wala si ya mabaya, kuwapa ninyi tumaini siku zenu za mwisho.”

Hata hivyo ni Muhimu kufahamu kuwa kama Mungu baba yetu wa Mbinguni amekusudia kutuheshimisha sisi, ieleweke wazi kuwa shetani atapambana kwa kila namna kuhakikisha ya kuwa heshima hiyo inaharibiwa vazi la heshima ambalo Mungu anataka kukuvisha linaweza kuwa sababu kubwa sana ya vita vyako duniani lakini kumbuka wakati wote kusudi la Mungu ndilo litakalosimama

Kuharibiwa kwa vazi la Yusufu!

Tumejifunza na kuona kuwa vazi hili tayari kinabii linaashiria heshima ambayo Mungu amekusudia Kumpa Yusufu, lakini vilevile ni heshima ambayo Mungu amekusudia kumpa kila mmoja wetu, ni muhimu kufahamu kuwa kusudi kubwa la ibilisi au shetani ambaye ni adui wa makusudi yote ya Mungu ndani yetu ni pamoja na kupambana na ile Heshima ambayo Mungu ameikusudia katika maisha yetu, na hii ni kutaka kuiharibu na kuichafua ile heshima ili yamkini aweze kupambana na kusudi la Mungu lililoko ndani yetu, ona mfululizo wa matukio magumu unaambatana na maisha ya Yusufu yote yakilenga kuharibu vazi lake kusalitiwa, kuchukiwa bila sababu, kupanwa kuuawa au kuuzwa uhamishoni  na jambo la kwanza ilikuwa ni kumbua lile vazi.

Mwanzo 37:23-24 “Ikawa Yusufu alipofika kwa ndugu zake, wakamvua Yusufu kanzu yake, kanzu ile ndefu aliyoivaa, wakamtwaa wakamtupa katika birika; na hiyo birika ilikuwa tupu, hamna maji.”

Unaweza kuona chuki dhidi ya Yusufu haikuwa juu yake mwenyewe tu lakini ilikuwa na juu ya ile kanzu, vita kali ilikuwa dhidi ya vazi la Yusufu, na Nduguze hawakuishia hapo tu walihakikisha kuwa wanaliharibu vazi lile na kumtumia salamu baba yake ili yamkini naye aweze kujuta kwa kumuandalia Yusufu vazi kama lile ona

Mwanzo 37:31-34 “Wakaitwaa kanzu ya Yusufu, wakachinja mwana-mbuzi, na kuichovya kanzu katika damu. Wakaenda nayo ile kanzu ndefu, wakamletea baba yao, wakasema, Tumeona hii; basi, utambue kama kanzu hii ni ya mwanao, ama siyo. Akaitambua, akasema, Ndiyo kanzu ya mwanangu, mnyama mkali amemla; bila shaka Yusufu ameraruliwa. Yakobo akararua mavazi yake, akajivika gunia viunoni, na kumlilia mwanawe siku nyingi.”

Unaona kimsingi chuki, na husuda juu ya Yusufu kwa ndugu zake haikutokana na nafsi zao tu kwani wao walimalizia hapo, lakini ni wazi kuwa chuki hii inatoka kwa yule adui, adui hana mpango mwema na vazi la Yusufu la aina yoyote ile fikiria kuwa ameuzwa ugenini utumwani, huko nako hakuna mtu anayeijua historia yake wala ndoto yake na kwa vile Mungu alikuwa amemkusudia kuwa msimamizi na kiongozi anajikuta utumwani ananunuliwa na Potifa naye anamfanya kuwa mtu mkubwa katika nyumba yake ona  

Mwanzo 39:1-18 “Basi Yusufu akaletwa mpaka Misri naye Potifa, akida wa Farao, mkuu wa askari, mtu wa Misri, akamnunua mkononi mwa hao Waishmaeli waliomleta huko. BWANA akawa pamoja na Yusufu, naye akasitawi; naye alikuwa katika nyumba ya bwana wake, yule Mmisri. Bwana wake akaona ya kwamba BWANA yu pamoja naye, na ya kuwa BWANA anafanikisha mambo yote mkononi mwake. Yusufu akaona neema machoni pake, akamtumikia. Naye akamweka awe msimamizi juu ya nyumba yake, na yote yaliyomo akayaweka mkononi mwake. Ikawa tokea wakati alipomweka awe msimamizi juu ya nyumba yake, na vyote vilivyomo, BWANA akabariki nyumba ya yule Mmisri kwa ajili ya Yusufu. Mbaraka wa BWANA ukawa juu ya vyote alivyokuwa navyo katika nyumba, na katika shamba. Akayaacha yote aliyokuwa nayo mkononi mwa Yusufu; wala hakujua habari za kitu cho chote chake, ila hicho chakula alichokula tu. Ikawa baada ya mambo hayo, mke wa bwana wake akamtamani Yusufu, akamwambia, Lala nami. Lakini akakataa, akamwambia mke wa bwana wake, Tazama, bwana wangu hajui kitu kilichowekwa kwangu nyumbani, na vyote alivyo navyo amevitia mkononi mwangu. Hakuna mkuu katika nyumba hii kuliko mimi, wala hakunizuilia kitu cho chote ila wewe, kwa kuwa wewe u mkewe. Nifanyeje ubaya huu mkubwa nikamkose Mungu?  Akawa akizidi kusema na Yusufu siku baada ya siku, lakini hakumsikia alale naye, wala aongee naye. Ikawa, siku moja, akaingia nyumbani atende kazi yake, wala hapakuwa na mtu katika watu wa nyumbani humo ndani; huyo mwanamke akamshika nguo zake, akisema, Lala nami. Yusufu akaiacha nguo yake mkononi mwake, akakimbia, akatoka nje. Ikawa alipoona ya kwamba amemwachilia nguo yake mkononi mwake, naye amekimbia nje, akawaita watu wa nyumbani mwake, akasema nao, akinena, Angalieni, ametuletea mtu Mwebrania atufanyie dhihaka. Ameingia kwangu, ili alale nami, nikalia kwa sauti kuu. Ikawa, aliposikia ya kuwa nimepaza sauti yangu na kulia, aliiacha nguo yake kwangu, akakimbia, akatoka nje. Basi akaiweka ile nguo kwake hata bwana wake aje nyumbani. Naye akamwambia kama maneno hayo, akisema, Yule mtumwa Mwebrania uliyemleta kwetu, aliingia kwangu anidhihaki. Ikawa nilipopaza sauti yangu, nikalia, akaacha nguo yake kwangu akakimbia nje.”

Unapoendelea kufuatilia maisha ya Yusufu hata kule ugenini utakubaliana nani kwamba sio ndugu zake tu, lakini ni shetani anahusika kufuatilia vazi la Yusufu kwani hata watu wasiomjua wageni bado waliendelea kuandama nguo au vazi jingine la Yusufu katika nyumba ya Potifa ili waharibu kile ambacho Mungu amekikusudia,  makusudi ni kuwa maisha ya Yusufu yawe matatani na asipate nafasi kabisa ya kulitumikia shuri la Mungu, vazi la pili la yusufu linaingia matatani sasa Yusufu ana mavazi ya kifungwa gerezani hata hivyo bado neema ya Mungu ilikuwa pamoja naye hata akiwako kule gerezani  kwa kuwa yeye ana karama ya usimamizi ona

Mwanzo 39:21-23 “Lakini BWANA akawa pamoja na Yusufu, akamfadhili, akampa kibali machoni pa mkuu wa gereza. Mkuu wa gereza akawatia mkononi mwa Yusufu watu wote waliofungwa, waliomo gerezani; na yote yaliyofanyika humo ndiye aliyeyafanya. Wala mkuu wa gereza hakuangalia neno lililoko mkononi mwa Yusufu; kwa kuwa BWANA alikuwa pamoja naye. BWANA akayafanikisha yote aliyoyafanya

Yusufu katika vazi jipya

Hata pamoja na mapito yote aliyoyapitia Yusufu Bado Mungu alikuwa Pamoja naye, Mungu atakuwa pamoja nasi wakati wote katika kuhakikisha ya kuwa mpango wake unatimizwa kwetu, Yusufu hatimaye aliweza kutumia kipawa chake kutafasiri ndoto na hatimaye alitafasiri ndoto ya Farao ambayo ilimpatia nafasi kubwa sana na akalitimiza kusudi la Mungu

Mwanzo 41:39-44 “Farao akamwambia Yusufu, Kwa kuwa Mungu amekufahamisha hayo yote, hapana mwenye akili na hekima kama wewe. Basi wewe utakuwa juu ya nyumba yangu, na kwa neno lako watu wangu watatawaliwa. Katika kiti cha enzi tu nitakuwa mkuu kuliko wewe. Farao akamwambia Yusufu, Tazama, nimekuweka juu ya nchi yote ya Misri. Farao akavua pete yake ya muhuri mkononi mwake, akaitia mkononi mwa Yusufu; akamvika mavazi ya kitani nzuri, na kumtia mkufu wa dhahabu shingoni mwake. Akampandisha katika gari lake la pili alilokuwa nalo. Na watu wakapiga kelele mbele yake, Pigeni magoti. Hivyo akamweka juu ya nchi yote ya Misri. Farao akamwambia Yusufu, Mimi ni Farao, na bila amri yako, mtu asiinue mkono wala mguu katika nchi yote ya Misri.”

Kumbe wote tunaweza kukubaliana wazi kuwa vazi la Yusufu lilikuwa lina uhusiano mkubwa sana na nafasi aliyokuwa nayo, Mungu alikuwa amekusudia kutimiza kusudi Fulani ndani yake Sasa sio baba yake tu wala sio Mungu pekee farao pia anamvika mavazi Yusufu kutoka gerezani saa anavikwa mavazi ya kifalme anapewa na mamlaka ili aweze kutimiza hivyo kusudi kubwa la Mungu

Mambo ya kujifunza kutoka katika vazi la Yusufu

1.       Vazi la sifa njema – Yusufu alitengenezewa vazi la kwanza na Baba yake kwa sababu alikuwa ni mtoto mwenye sifa njema kuliko wengine alipata kibali kwa baba yake, alipata neema ni vazi la upendeleo, ni sifa hii njema iliyoweza kuinua chuki na ibilisi alikusudia kuiharibu,

 

Mwanzo 37:3-4 “Basi Israeli akampenda Yusufu kuliko wanawe wote, maana ni mwana wa uzee wake, akamfanyia kanzu ndefu. Ndugu zake wakaona ya kuwa baba yao anampenda kuliko ndugu zake wote, wakamchukia, wala hawakuweza kusema naye kwa amani.”

 

Yusufu alifanyiwa hila nyingi sana za kibinadamu kupitia ndugu zake lakini tunajifunza ya kuwa kusudi la Bwana ndilo litakalosimama, ikiwa Mungu amekukusudia Heshima hata iwe gerezani heshima yako itabaki pale pale

 

Mithali 19:21 “Mna hila nyingi moyoni mwa mtu; Lakini shauri la Bwana ndilo litakalosimama.”Mavazi yake yalichafuliwa lakini Mungu alimvisha mavazi ya Kimisri na kumuinua juu akitumia farasi wa farao na Pete ya farao, Nataka nikuhakikishie ya kuwa ukisimama na Mungu hakuna mtu atafanikiwa katika hila yake ya aina yoyote.

 

2.       Vazi la utumwa – Ni ukweli ulio wazi kuwa vazi la Yusufu ilichanwa chanwa na kuharibiwa na kuchafuliwa kwa damu na Yakobo alionyeshwa ili atambue kama kanzu ile ni ya mwanaye Mwanzo 37:31-34 “Wakaitwaa kanzu ya Yusufu, wakachinja mwana-mbuzi, na kuichovya kanzu katika damu. Wakaenda nayo ile kanzu ndefu, wakamletea baba yao, wakasema, Tumeona hii; basi, utambue kama kanzu hii ni ya mwanao, ama siyo. Akaitambua, akasema, Ndiyo kanzu ya mwanangu, mnyama mkali amemla; bila shaka Yusufu ameraruliwa. Yakobo akararua mavazi yake, akajivika gunia viunoni, na kumlilia mwanawe siku nyingi.”

 

Yusufu alipata vazi lingine huko utumwani alinunuliwa kama mtumwa wa amrijeshi mkuu wa farao alivikwa mavazi ya kitumwa ili amtumikie mtu, lilikuwa vaza la anasa na lilikuwa vazi la tama lakini Yusufu aliishinda tamaa, aliushinda ulimwengu, alimuheshimu Mungu hata katika mazingira magumu nay a ugenini, Mungu huwaheshimu wale wanaomuheshimu  Yusufu alimuheshimu Mungu kila alipokuwepo, alitambua ya kuwa anapaswa kuwa mwaminifu kwa wanadamu na kwa Mungu pia, aliikataa dhambi nimtendeje Bwana Mungu wangu dhambi kubwa namna hii, aliamua kumuheshimu Mungu katika maisha yake alijihami na ubaya wa kila namna na kwa sababu hiyo hatimaye kwa uvumilivu mkubwa alivuna matunda yake yaliyokusudiwa

 

1Samuel 2:30 “Kwa sababu hiyo, Bwana, Mungu wa Israeli, asema, Ni kweli, nalisema ya kuwa nyumba yako, na nyumba ya baba yako itakwenda mbele zangu milele; lakini sasa Bwana asema, Jambo hili na liwe mbali nami; kwa maana wao wanaoniheshimu nitawaheshimu, na wao wanaonidharau watahesabiwa kuwa si kitu.”

 

3.       Vazi la Heshima – lolote linalotokea katika maisha yetu liko chini ya utawala wa Mungu hata pale watu wanapotutendea uovu na hila tukumbuke tu ya kuwa Mungu ndiye anayetawala, Pamoja na mapito yote uaminifu na uvumilivu ulimleta Yusufu katika heshima kubwa sana alivikwa mavazi ya kifahari na kuinuliwa na watu wote kuinamaa mbele zake ona

 

Mwanzo 41:41-42 “Farao akamwambia Yusufu, Tazama, nimekuweka juu ya nchi yote ya Misri. Farao akavua pete yake ya muhuri mkononi mwake, akaitia mkononi mwa Yusufu; akamvika mavazi ya kitani nzuri, na kumtia mkufu wa dhahabu shingoni mwake.”

Hitimisho:

Mungu anao mpango Madhubuti wa kumuheshimu kila mmoja wetu, ni wajhibu wako kuhakikisha ya kuwa unatunza sifa njema ulizonazo, huku ukitambua ya kuwa, Shetani atakupiga vita akiwatumia watu, jilinde na kuhakikisha kuwa unaendelea kuyatunza maisha yako, haijalishi ni mapitio magumu kiasi gani unayapitia.haijalishi uko sehemu ya ugenini ambako watu hawakuoni kumbuka ya kuwa Mungu anakuona na anataka wewe umuonyeshe heshima na Mungu atakuwa pamoja nawe  Mpango wake Mungu ni kutaka kukuheshimu na Mungu analo vazi, anao farasi anayo mavazi na anao watakaokutangaza pale utakapoitunza heshima inayokusudiwa kwako na Mungu na wazazi wako na ulimwengu , Bado Mungu anamkusudia kila mmoja wetu kuvikwa mavazi ya heshima kubwa

Esta 6:7-10 “Basi Hamani akaingia. Mfalme akamwambia, Afanyiziwe nini yule ambaye mfalme apenda kumheshimu? Hamani akasema moyoni mwake, Ni nani ambaye mfalme apenda kumheshimu kuliko mimi? Basi Hamani akamwambia mfalme, Yule ambaye mfalme apenda kumheshimu, na aletewe mavazi ya kifalme ambayo mfalme amezoea kuyavaa, na farasi ambaye mfalme humpanda mwenyewe, ambaye ametiwa taji ya kifalme kichwani; na yale mavazi na yule farasi akabidhiwe mkononi mmojawapo wa maakida wa mfalme aliye mstahiki; ili makusudi amvike yule ambaye mfalme apenda kumheshimu, na kumrakibisha juu ya farasi kuipitia njia kuu ya mjini, na kupiga mbiu mbele yake, kusema, Hivyo ndivyo atakavyofanyiziwa mtu yule ambaye mfalme apenda kumheshimu. Basi mfalme akamwambia Hamani, Hima! Twaa mavazi na farasi kama ulivyosema, ukamfanyizie vivyo hivyo Mordekai, Myahudi, aketiye mlangoni pa mfalme; lisipungue neno lo lote katika yote uliyoyasema.” Ni ahadi ya Mungu kwamba kila mtu atakayeshida tapata heshima kubwa sio hapa duniani tu bali na mbinguni pia

Ufunuo 3:5 “Yeye ashindaye atavikwa hivyo mavazi meupe, wala sitalifuta kamwe jina lake katika kitabu cha uzima, nami nitalikiri jina lake mbele za Baba yangu, na mbele ya malaika zake.”

Na Rev. Innocent Samuel Kamote

Mkuu wa wajenzi mwenye Hekima!

Hakuna maoni: